RUTHU
1 Basi katika siku ambazo waamuzi+ walikuwa wakitekeleza hukumu,* kulikuwa na njaa kali nchini; na mwanamume fulani akatoka Bethlehemu+ huko Yuda akahamia katika mashamba ya* Moabu akiwa mgeni,+ yeye, pamoja na mke wake, na watoto wake wawili wa kiume. 2 Mwanamume huyo aliitwa Elimeleki,* na mke wake aliitwa Naomi,* na watoto wake wawili waliitwa Maloni* na Kilioni.* Walikuwa Waefrathi kutoka Bethlehemu nchini Yuda. Wakafika katika mashamba ya Moabu na kuishi huko.
3 Baada ya muda, Elimeleki mume wa Naomi akafa, naye akabaki na wanawe wawili. 4 Baadaye wana hao wakaoa wanawake Wamoabu; mmoja aliitwa Orpa, na mwingine aliitwa Ruthu.+ Waliishi huko kwa miaka kumi hivi. 5 Kisha wana hao wawili, Maloni na Kilioni wakafa pia, Naomi akabaki bila watoto wake wawili na bila mume wake. 6 Akaanza safari kutoka katika mashamba ya Moabu pamoja na binti wakwe zake, kwa maana akiwa Moabu alisikia kwamba Yehova alikuwa amewaelekezea uangalifu watu Wake kwa kuwapa chakula.*
7 Akaondoka mahali alipokuwa akiishi pamoja na binti wakwe zake wawili. Walipokuwa wakitembea njiani kurudi katika nchi ya Yuda, 8 Naomi akawaambia: “Nendeni, rudini kila mmoja wenu nyumbani kwa mama yake. Yehova na awatendee kwa upendo mshikamanifu,+ kama tu mlivyowatendea waume zenu ambao wamekufa na kama mlivyonitendea mimi. 9 Yehova na awabariki* ili kila mmoja wenu apate usalama* katika nyumba ya mume wake.”+ Kisha akawabusu, nao wakalia kwa sauti kubwa. 10 Wakamwambia tena na tena: “Hapana, tutaenda nawe kwa watu wako.” 11 Lakini Naomi akawaambia: “Rudini binti zangu. Kwa nini mnifuate? Je, ninaweza tena kuzaa watoto ambao watakuwa waume zenu?+ 12 Rudini, binti zangu. Nendeni, kwa maana nimezeeka sana siwezi kuolewa tena. Hata kama ningetumaini kupata mume usiku wa leo na kuzaa watoto pia, 13 je, mngeendelea kuwangojea ili wakue? Je, mngekataa kuolewa tena mkiwasubiri? Hapana, binti zangu, nina uchungu mwingi kwa ajili yenu, kwa sababu mkono wa Yehova umegeuka dhidi yangu.”+
14 Wakalia tena kwa sauti kubwa, kisha Orpa akambusu mama mkwe wake na kwenda zake. Lakini Ruthu akashikamana naye. 15 Kwa hiyo Naomi akamwambia: “Tazama! Dada mkwe mwenzako mjane amerudi kwa watu wake na kwa miungu yake. Rudi pamoja na dada mkwe mwenzako.”
16 Lakini Ruthu akasema: “Usinisihi nikuache, nirudi na kuacha kukufuata; kwa maana mahali utakapoenda nitaenda, na mahali utakapolala usiku hapo ndipo nitakapolala pia. Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.+ 17 Mahali utakapokufa nitafia hapo, na hapo ndipo nitakapozikwa. Yehova na aniadhibu, tena vikali, ikiwa kitu chochote kitanitenganisha nawe isipokuwa kifo.”
18 Naomi alipoona kwamba Ruthu anasisitiza kwenda naye, hakuendelea kumsihi asimfuate. 19 Wote wawili wakaendelea na safari mpaka walipofika Bethlehemu.+ Mara tu walipofika Bethlehemu, jiji lote likasisimka kwa sababu yao, na wanawake wakaulizana: “Je, huyu ni Naomi?” 20 Naye aliwaambia: “Msiniite Naomi.* Niiteni Mara,* kwa maana Mweza-Yote amefanya maisha yawe machungu sana kwangu.+ 21 Mikono yangu ilikuwa imejaa nilipoenda, lakini Yehova amenifanya nirudi mikono mitupu. Kwa nini mniite Naomi, wakati Yehova ndiye aliyenipinga na Mweza-Yote ndiye aliyeniletea msiba?”+
22 Hivyo ndivyo Naomi alivyorudi kutoka katika mashamba ya Moabu+ pamoja na Ruthu, binti mkwe wake Mmoabu. Walifika Bethlehemu mwanzoni mwa mavuno ya shayiri.+
2 Basi Naomi alikuwa na mtu wa ukoo wa Elimeleki, mume wake; mtu huyo aliitwa Boazi+ na alikuwa tajiri sana.
2 Ruthu Mmoabu akamwambia Naomi: “Tafadhali, niruhusu niende mashambani nikaokote masalio+ ya masuke ya nafaka nyuma ya yeyote yule atakayeniruhusu.” Basi Naomi akamwambia: “Nenda, binti yangu.” 3 Basi akaenda na kuanza kuokota masalio mashambani nyuma ya wavunaji. Bila kutarajia akajikuta katika shamba la Boazi,+ aliyekuwa wa ukoo wa Elimeleki.+ 4 Ndipo Boazi akaja kutoka Bethlehemu na kuwaambia wavunaji: “Yehova na awe pamoja nanyi.” Nao wakajibu: “Yehova na akubariki.”
5 Kisha Boazi akamuuliza kijana aliyekuwa msimamizi wa wavunaji: “Msichana huyu ni wa nani?” 6 Kijana aliyekuwa msimamizi wa wavunaji akamjibu: “Msichana huyu ni Mmoabu,+ aliyerudi na Naomi kutoka katika mashamba ya Moabu.+ 7 Aliniuliza, ‘Tafadhali, ninaweza kuokota+ na kukusanya masuke* ya nafaka yaliyoachwa na wavunaji?’ Amekuwa akifanya kazi tangu alipokuja asubuhi, ni sasa tu ameketi kibandani ili kupumzika kidogo.”
8 Kisha Boazi akamwambia Ruthu: “Sikiliza, binti yangu. Usiende kuokota masalio katika shamba lingine, wala usiende mahali pengine popote; uwe karibu na wafanyakazi wangu wasichana.+ 9 Angalia shamba wanalovuna, nawe uwafuate. Nimewaamuru wale vijana wa kiume wasikuguse.* Ukihisi kiu, nenda kwenye mitungi ya maji ukanywe maji yaliyotekwa na hao vijana.”
10 Ndipo Ruthu akapiga magoti na kuinama mpaka chini na kumwambia: “Nimepataje kibali machoni pako, na kwa nini umenijali ilhali mimi ni mgeni?”+ 11 Boazi akamjibu: “Nimeambiwa mambo yote uliyomfanyia mama mkwe wako baada ya mume wako kufa na jinsi ulivyomwacha baba yako na mama yako na nchi ya watu wako wa ukoo ukaja kwa watu ambao hukuwajua.+ 12 Yehova na akuthawabishe kwa yale uliyofanya,+ na upate malipo* kamili kutoka kwa Yehova Mungu wa Israeli, ambaye umekuja kutafuta kimbilio chini ya mabawa yake.”+ 13 Basi Ruthu akasema: “Acha nipate kibali machoni pako, bwana wangu, kwa sababu umenifariji na kunitia moyo,* ingawa mimi hata si mmoja wa watumishi wako.”
14 Wakati wa chakula, Boazi akamwambia: “Njoo hapa, ule mkate na kuuchovya katika siki.” Basi Ruthu akaketi kando ya wavunaji. Boazi akampa nafaka zilizokaangwa, akala, akashiba, na kubakiza. 15 Aliposimama ili aokote masuke ya nafaka,+ Boazi akawaamuru hivi watumishi wake: “Mwacheni aokote masuke* ya nafaka yaliyokatwa pia, msimtese.+ 16 Pia, hakikisheni kwamba mnachomoa masuke machache kutoka katika matita na kumwachia nyuma ili ayaokote, msimkataze.”
17 Basi akaendelea kuokota masuke shambani mpaka jioni.+ Alipoyapura, alipata karibu efa* moja ya shayiri. 18 Halafu akachukua nafaka hiyo na kwenda jijini, na mama mkwe wake akaona nafaka aliyokuwa ameokota. Halafu Ruthu akachukua chakula alichokuwa amebakiza+ baada ya kula na kushiba, akampa.
19 Basi mama mkwe wake akamuuliza: “Leo uliokota masuke wapi? Ulifanya kazi wapi? Na abarikiwe yule aliyekutendea kwa fadhili.”+ Ndipo akamwambia mama mkwe wake kuhusu mtu aliyefanya kazi katika shamba lake: “Nilifanya kazi katika shamba la mwanamume anayeitwa Boazi.” 20 Basi Naomi akamwambia binti mkwe wake: “Na abarikiwe na Yehova, ambaye hajawahi kamwe kukosa kuwatendea kwa upendo mshikamanifu walio hai na waliokufa.”+ Naomi akaendelea kusema: “Mwanamume huyo ni mtu wetu wa ukoo.+ Yeye ni kati ya watu wanaoweza kutukomboa.”*+ 21 Ndipo Ruthu Mmoabu akasema: “Pia aliniambia, ‘Uwe karibu na watumishi wangu mpaka watakapomaliza kuvuna mavuno yangu yote.’”+ 22 Naomi akamwambia Ruthu binti mkwe wake: “Binti yangu, ni afadhali ufuatane na wafanyakazi wake wasichana, usije ukasumbuliwa katika shamba lingine.”
23 Kwa hiyo akafuatana na wasichana wa Boazi na kuokota masuke mpaka mwisho wa mavuno ya shayiri+ na mavuno ya ngano. Naye akaendelea kuishi na mama mkwe wake.+
3 Basi Naomi mama mkwe wake akamwambia: “Binti yangu, je, si vema nikutafutie makao*+ ili mambo yakuendee vyema? 2 Boazi, ambaye ulifanya kazi na wasichana wake, je, yeye si mtu wetu wa ukoo?+ Usiku wa leo anapepeta shayiri kwenye uwanja wa kupuria. 3 Basi oga na ujipake mafuta yenye marashi; kisha uvae vizuri na kwenda kwenye uwanja wa kupuria. Hakikisha hakuoni hadi atakapomaliza kula na kunywa. 4 Atakapolala, angalia mahali ambapo atalala; kisha uende ufunue miguu yake na ulale hapo. Atakwambia jambo unalopaswa kufanya.”
5 Basi Ruthu akasema: “Yote unayoniambia nitafanya.” 6 Kwa hiyo, akaenda kwenye uwanja wa kupuria na kufanya yote aliyoambiwa na mama mkwe wake. 7 Basi Boazi akala, akanywa, na kuchangamka moyoni. Kisha akaenda kulala mwisho wa rundo la nafaka. Kisha Ruthu akaja kimyakimya, akamfunua miguu, na kulala hapo. 8 Katikati ya usiku, mwanamume huyo alianza kutetemeka, akaketi na kumwona mwanamke amelala miguuni pake. 9 Akamuuliza: “Wewe ni nani?” Akajibu: “Mimi ni Ruthu, kijakazi wako. Nifunike mimi kijakazi wako kwa vazi lako,* kwa maana wewe ni mkombozi.”+ 10 Basi Boazi akasema: “Yehova na akubariki, binti yangu. Wakati huu, umetenda kwa upendo mshikamanifu zaidi kuliko mwanzoni,+ kwa kuwa hukuwafuata wale vijana, matajiri au maskini. 11 Na sasa binti yangu, usiogope. Nitakufanyia kila jambo utakalosema,+ kwa maana kila mtu jijini* anajua kwamba wewe ni mwanamke bora. 12 Ni kweli kwamba mimi ni mkombozi,+ lakini kuna mkombozi ambaye ni mtu wa karibu zaidi wa ukoo kuliko mimi.+ 13 Kaa hapa usiku wa leo, na ikiwa atakukomboa asubuhi, ni sawa! Na akukomboe.+ Lakini ikiwa hataki kukukomboa, kwa hakika kama Yehova anavyoishi, mimi mwenyewe nitakukomboa. Lala hapa mpaka asubuhi.”
14 Basi akalala miguuni pake mpaka asubuhi, kisha akaamka kabla ya mapambazuko wakati ambapo ni vigumu kumtambua yeyote. Boazi akasema: “Isijulikane kwamba mwanamke alikuja kwenye uwanja wa kupuria.” 15 Naye akaendelea kusema: “Kilete kitambaa ulichojifunika ukitandaze.” Basi Ruthu akakitandaza, naye Boazi akampimia vipimo sita* vya shayiri na kumtwika, kisha Boazi akaenda jijini.
16 Ruthu akaenda kwa mama mkwe wake, ambaye alimuuliza: “Mambo yaliendaje,* binti yangu?” Akamwambia yote ambayo mwanamume huyo alimtendea. 17 Tena akasema: “Alinipa vipimo hivi sita vya shayiri na kuniambia, ‘Usiende kwa mama mkwe wako mikono mitupu.’” 18 Basi Naomi akamwambia: “Kaa hapa binti yangu, mpaka utakapojua jinsi itakavyokuwa, kwa maana mwanamume huyo hatapumzika mpaka atakapotimiza jambo hilo leo.”
4 Sasa Boazi akapanda kwenda kwenye lango la jiji+ na kuketi hapo. Na tazama! yule mkombozi ambaye Boazi alimtaja+ alikuwa akipita. Basi Boazi akamwita: “Fulani wa fulani, njoo, keti hapa.” Akaja na kuketi. 2 Kisha Boazi akawaita wazee kumi wa jiji,+ akawaambia: “Ketini hapa.” Nao wakaketi.
3 Ndipo Boazi akamwambia mkombozi huyo:+ “Naomi aliyerudi kutoka katika mashamba ya Moabu+ hana budi kuuza shamba la ndugu yetu Elimeleki.+ 4 Niliona nikufahamishe jambo hilo na kukwambia, ‘Linunue mbele ya wakaaji na wazee wa watu wangu.+ Ikiwa utalikomboa, likomboe. Lakini ikiwa hutalikomboa, niambie ili nijue, kwa maana una haki ya kulikomboa, mimi ni wa pili.’” Mtu huyo akasema: “Niko tayari kulikomboa.”+ 5 Kisha Boazi akamwambia: “Siku utakapolinunua shamba hilo kutoka kwa Naomi, unapaswa kulinunua pia kutoka kwa Ruthu Mmoabu, mke wa mwanamume aliyekufa, ili kurudisha jina la mume wake aliyekufa katika urithi huo.”+ 6 Basi mkombozi huyo akasema: “Siwezi kulikomboa kwa maana huenda nikaharibu urithi wangu mwenyewe. Likomboe kwa ajili yako mwenyewe ukitumia haki yangu ya kukomboa, kwa sababu siwezi kulikomboa.”
7 Ili kuhalalisha makubaliano yoyote, hii ndiyo desturi iliyofuatwa zamani katika Israeli kuhusu haki ya kukomboa na kubadilishana vitu: Mtu alipaswa kuvua kiatu chake+ na kumpa mwenzake, na huo ndio utaratibu uliofuatwa ili kuthibitisha* makubaliano katika Israeli. 8 Kwa hiyo mkombozi huyo alivua kiatu alipomwambia Boazi, “Linunue liwe lako.” 9 Kisha Boazi akawaambia wazee na watu wote waliokuwepo: “Ninyi ni mashahidi+ leo kwamba ninanunua kutoka kwa Naomi vitu vyote vilivyokuwa vya Elimeleki na vitu vyote vilivyokuwa vya Kilioni na Maloni. 10 Namchukua pia Ruthu Mmoabu, mke wa Maloni, awe mke wangu ili kurudisha jina la mwanamume huyo aliyekufa katika urithi wake,+ ili jina la mwanamume huyo aliyekufa lisifutiliwe mbali kutoka kati ya ndugu zake na kutoka katika lango la jiji lake. Ninyi ni mashahidi leo.”+
11 Ndipo watu wote waliokuwa katika lango la jiji na wale wazee wakasema: “Sisi ni mashahidi! Yehova na ambariki mke anayekuja nyumbani mwako ili awe kama Raheli na Lea, ambao walijenga nyumba ya Israeli.+ Ufanikiwe katika Efratha+ na ujijengee jina zuri* katika Bethlehemu.+ 12 Nyumba yako na iwe kama nyumba ya Perezi,+ ambaye Tamari alimzalia Yuda, kupitia uzao ambao Yehova atakupa kutoka kwa mwanamke huyu kijana.”+
13 Basi Boazi akamwoa Ruthu. Akalala naye, na Yehova akamwezesha kupata mimba na kuzaa mwana. 14 Halafu wanawake wakamwambia Naomi: “Yehova na asifiwe, ambaye hakukuacha bila mkombozi leo. Jina la mwana huyo na litangazwe katika Israeli! 15 Yeye* amekurudishia uhai wako* na atakutunza uzeeni, kwa sababu amezaliwa na binti mkwe wako anayekupenda+ na ambaye ni bora kwako kuliko wana saba.” 16 Naomi akamchukua mtoto huyo na kumbeba kifuani, naye akamtunza.* 17 Kisha wanawake majirani wakampa jina. Wakasema, “Naomi amezaa mwana,” nao wakamwita Obedi.+ Yeye ndiye baba ya Yese,+ aliyemzaa Daudi.
18 Basi huu ndio ukoo wa* Perezi:+ Perezi alimzaa Hezroni;+ 19 Hezroni akamzaa Ramu; Ramu akamzaa Aminadabu;+ 20 Aminadabu+ akamzaa Nashoni; Nashoni akamzaa Salmoni; 21 Salmoni akamzaa Boazi; Boazi akamzaa Obedi; 22 Obedi akamzaa Yese;+ na Yese akamzaa Daudi.+
Tnn., “wakihukumu.”
Au “eneo la.”
Maana yake “Mungu Wangu Ni Mfalme.”
Maana yake “Uzuri Wangu.”
Labda linatokana na neno la Kiebrania linalomaanisha “kuwa dhaifu; kuwa mgonjwa.”
Maana yake “Anayeshindwa; Anayefikia Mwisho.”
Tnn., “mkate.”
Tnn., “awape zawadi.”
Tnn., “apate mahali pa kupumzika.”
Maana yake “Uzuri Wangu.”
Maana yake “Uchungu.”
Au labda, “matita.”
Au “wasikusumbue.”
Au “thawabu.”
Tnn., “umezungumza na moyo wangu.”
Au labda, “matita.”
Karibu kilogramu 13. Angalia Nyongeza B14.
Au “mmojawapo wa watu wetu wa ukoo walio na haki ya kutukomboa.”
Tnn., “mahali pa kumpumzika.”
Au “pindo la vazi lako.”
Tnn., “katika lango lote la watu wangu.”
Labda vipimo sita vya sea, au karibu kilogramu 20. Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “Wewe ni nani?”
Au “kutoa ushuhuda wa.”
Tnn., “utangaze jina.”
Yaani, mjukuu wa Naomi.
Au “nafsi yako.”
Au “akawa mlezi wake.”
Tnn., “hivi ndivyo vizazi vya.”