Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt Mika 1:1-7:20
  • Mika

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mika
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Mika

MIKA

1 Neno la Yehova lililomjia Mika*+ wa Moreshethi, katika siku za utawala wa Yothamu,+ Ahazi,+ na Hezekia,+ wafalme wa Yuda,+ na ambalo alilipokea katika maono kuhusu Samaria na Yerusalemu:

 2 “Sikieni, enyi mataifa yote!

Sikiliza, Ee dunia na vitu vyote vinavyokujaza,

Acha Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova awe shahidi dhidi yako+

—Yehova kutoka katika hekalu lake takatifu.

 3 Kwa maana tazama! Yehova anatoka mahali pake;

Atashuka chini na kukanyaga sehemu za juu za dunia.

 4 Milima itayeyuka chini yake,+

Na mabonde yatagawanyika*

Kama nta mbele ya moto,

Kama maji yanayomwagwa kwenye mteremko mkali.

 5 Hayo yote kwa sababu ya uasi wa Yakobo,

Kwa sababu ya dhambi za nyumba ya Israeli.+

Uasi wa Yakobo ni nini?

Je, si Samaria?+

Na mahali pa juu pa Yuda ni nini?+

Je, si Yerusalemu?

 6 Nitafanya Samaria kuwa rundo la magofu la shambani,

Mahali pa kupanda mizabibu;

Nitayatupa* mawe yake chini bondeni,

Nami nitaichimbua misingi yake.

 7 Sanamu zake zote za kuchongwa zitavunjwa vipandevipande,+

Na zawadi zote alizopewa kwa sababu ya ukahaba wake zitateketezwa motoni.*+

Nitaharibu kabisa sanamu zake zote.

Kwa sababu alizikusanya kwa kutumia malipo ya ukahaba,

Nazo zitakuwa tena malipo ya makahaba.”

 8 Kwa sababu hiyo nitalia kwa sauti na kupiga mayowe;+

Nitatembea bila viatu nikiwa uchi.+

Nitalia kwa sauti kama mbwamwitu wanavyolia,

Na kuomboleza kama mbuni wanavyoomboleza.

 9 Kwa sababu jeraha lake haliwezi kuponywa;+

Limefika mpaka Yuda.+

Pigo limeenea mpaka kwenye lango la watu wangu, mpaka Yerusalemu.+

10 “Msitangaze hilo kule Gathi;

Msilie hata kidogo.

Kule Beth-afra* mgaegae mavumbini.

11 Vukeni mkiwa uchi na wenye aibu, enyi wakaaji* wa Shafiri.

Wakaaji wa Saanani hawajatoka nje.

Kutakuwa na kilio kikubwa kule Beth-ezeli, nacho hakitawasaidia.

12 Kwa maana wakaaji wa Marothi wamengojea mema,

Lakini mabaya yameshuka kutoka kwa Yehova mpaka kwenye lango la Yerusalemu.

13 Fungeni kundi la farasi kwenye gari la vita, enyi wakaaji wa Lakishi.+

Mlikuwa chanzo cha dhambi kwa binti ya Sayuni,

Kwa maana maasi ya Israeli yalipatikana ndani yako.+

14 Kwa hiyo mtampa Moresheth-gathi zawadi za kumuaga.*

Nyumba za Akzibu+ zilikuwa kitu cha udanganyifu kwa wafalme wa Israeli.

15 Bado nitawaletea mshindi,*+ enyi wakaaji wa Maresha.+

Utukufu wa Israeli utafika mpaka Adulamu.+

16 Nyoeni upara na kuzikata kabisa nywele zenu kwa ajili ya watoto wenu wapendwa.

Nyoeni upara kama wa tai,

Kwa maana wamechukuliwa kutoka kwenu na kupelekwa uhamishoni.”+

2 “Ole wao wanaopanga njama yenye kudhuru,

Wanaotunga maovu vitandani mwao!

Kunapopambazuka wanayatekeleza,

Kwa sababu wana uwezo wa kuyatekeleza.+

 2 Wanatamani mashamba na kuyanyakua;+

Pia nyumba, na kuzichukua;

Wanamlaghai mtu na kuchukua nyumba yake,+

Wanachukua urithi wa mtu.

 3 Kwa hiyo Yehova anasema hivi:

‘Sasa basi nakusudia kuiletea familia hii msiba+ ambao hamtaweza kuuepuka.*+

Hamtatembea tena kwa kiburi,+ kwa sababu utakuwa wakati wa msiba.+

 4 Siku hiyo watu watatunga methali kuwahusu,

Nao watawaombolezea kwa uchungu.+

Watasema: “Tumeangamizwa kabisa!+

Alisababisha fungu la watu wangu lichukuliwe na wengine—Lo! Amenipokonya!+

Amemgawia yule asiye mwaminifu mashamba yetu.”

 5 Kwa hiyo hamtakuwa na mtu wa kunyoosha kamba ya kupimia,

Wa kuigawa ardhi katika kutaniko la Yehova.

 6 Wanahubiri wakisema, “Acheni kuhubiri!”

“Hawapaswi kuhubiri mambo haya;

Hatutapatwa na aibu!”

 7 Je, inasemwa, Ee nyumba ya Yakobo, kwamba

“Roho ya Yehova imekosa subira?

Je, haya ndiyo matendo yake?”

Je, maneno yangu mwenyewe hayawanufaishi wale wanaotembea kwa unyoofu?

 8 Lakini hivi karibuni watu wangu mwenyewe wameinuka kama adui.

Mnalivua hadharani pambo la kifahari pamoja na* vazi

Kutoka kwa watu wanaopita bila wasiwasi, kama watu wanaorudi kutoka vitani.

 9 Mnawafukuza wanawake wa watu wangu kutoka katika nyumba zao zenye kupendeza;

Mnaondoa fahari yangu milele kutoka kwa watoto wao.

10 Inukeni mwende zenu, kwa sababu hapa si mahali pa kupumzika.

Kwa sababu ya uchafu,+ kuna maangamizi, maangamizi makubwa.+

11 Mtu akifuata upepo na udanganyifu na kusema uwongo huu:

“Nitawahubiria kuhusu divai na pombe,”

Basi atakuwa mhubiri anayewafaa kabisa watu hawa!+

12 Kwa hakika nitawakusanya ninyi nyote, enyi watu wa Yakobo;

Kwa kweli nitawakusanya pamoja wale wanaobaki wa Israeli.+

Kwa umoja nitawaweka kama kondoo zizini,

Kama kundi la kondoo katika malisho yake;+

Litakuwa na kelele za watu.’+

13 Yule anayevunja lango na kutoka atawatangulia;

Nao watavunja lango na kupitia langoni kwenda nje.+

Mfalme wao atapitia humo akiwatangulia,

Huku Yehova akiwaongoza.”+

3 Nilisema: “Sikieni, tafadhali, enyi viongozi wa Yakobo

Nanyi makamanda wa nyumba ya Israeli.+

Je, hampaswi kujua jambo lililo la haki?

 2 Lakini mnachukia mema+ na kupenda maovu;+

Mnawachuna ngozi watu wangu na kuondoa nyama kutoka kwenye mifupa yao.+

 3 Pia mnakula nyama ya watu wangu+

Na kuwachuna ngozi,

Mnapasua mifupa yao, na kuivunja vipandevipande,+

Kama kitu kinachopikwa ndani ya chungu,* kama nyama ndani ya chungu cha kupikia.

 4 Wakati huo watamlilia Yehova awasaidie,

Lakini hatawajibu.

Atauficha uso wake kutoka kwao wakati huo,+

Kwa sababu ya matendo yao maovu.+

 5 Yehova anasema hivi kuhusu manabii wanaowapotosha watu wake,+

Wanaotangaza ‘Amani!’+ huku wakitafuna* kwa meno yao+

Lakini wanaotangaza* vita dhidi ya yule asiyeweka kitu vinywani mwao:

 6 ‘Mtakuwa na usiku;+ hakutakuwa na maono;+

Mtakuwa na giza tu, hakutakuwa na uaguzi.*

Jua litatua kwa manabii,

Na mchana utageuka kuwa giza kwao.+

 7 Watu wanaoona maono wataaibishwa,+

Na wabashiri watakata tamaa.

Wote watalazimika kufunika masharubu,*

Kwa maana hakuna jibu kutoka kwa Mungu.’”

 8 Lakini mimi, nimejazwa nguvu kwa roho ya Yehova,

Nimejazwa haki na uwezo,

Ili nimwambie Yakobo uasi wake na Israeli dhambi yake.

 9 Sikieni jambo hili, tafadhali, enyi viongozi wa nyumba ya Yakobo

Nanyi makamanda wa nyumba ya Israeli,+

Mnaochukia haki na kupotosha mambo yote yaliyonyooka,+

10 Mnaojenga Sayuni kwa umwagaji wa damu na Yerusalemu kwa ukosefu wa uadilifu.+

11 Viongozi* wake huhukumu ili wapate rushwa,+

Makuhani wake hufundisha ili wapate malipo,+

Na manabii wake hufanya uaguzi* ili wapate pesa.*+

Na bado wanamwegemea Yehova,* wakisema:

“Je, Yehova hayuko pamoja nasi?+

Hakuna msiba utakaotupata.”+

12 Basi kwa sababu yenu,

Sayuni litalimwa kama shamba,

Yerusalemu litakuwa marundo ya magofu,+

Na mlima wa Nyumba* utakuwa kama vilima msituni.*+

4 Katika siku za mwisho,*

Mlima wa nyumba ya Yehova+

Utaimarishwa kabisa juu ya vilele vya milima,

Nao utainuliwa juu ya vilima,

Na mataifa yatamiminika kwenye mlima huo.+

 2 Na mataifa mengi yataenda na kusema:

“Njooni, twendeni juu kwenye mlima wa Yehova

Na kwenye nyumba ya Mungu wa Yakobo.+

Naye atatufundisha njia zake,

Nasi tutatembea katika vijia vyake.”

Kwa maana sheria itatoka* Sayuni,

Na neno la Yehova litatoka Yerusalemu.

 3 Atatekeleza hukumu miongoni mwa mataifa mengi+

Na kunyoosha* mambo kuhusiana na mataifa yenye nguvu yaliyo mbali.

Watafua panga zao ziwe majembe ya plau

Na mikuki yao iwe miundu.+

Taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine,

Wala hawatajifunza vita tena kamwe.+

 4 Wataketi,* kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake,+

Na hakuna yeyote atakayewaogopesha,+

Kwa maana kinywa cha Yehova wa majeshi kimesema hayo.

 5 Kwa maana mataifa yote yatatembea, kila taifa katika jina la mungu wake,

Lakini sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu+ milele na milele.

 6 “Siku hiyo,” asema Yehova,

“Nitamkusanya yule aliyekuwa akichechemea,

Na kumkusanya pamoja yule aliyetawanyika,+

Pamoja na wale niliowatesa.

 7 Nitamfanya yule aliyekuwa akichechemea abaki,+

Na yule aliyepelekwa mbali kuwa taifa lenye nguvu;+

Na Yehova atawatawala akiwa mfalme katika Mlima Sayuni,

Kuanzia sasa mpaka milele.

 8 Lakini wewe, Ee mnara wa kundi,

Kilima cha binti ya Sayuni,+

Kwako wewe utakuja, naam, utawala wa kwanza* utakuja,+

Ufalme ambao ni wa binti ya Yerusalemu.+

 9 Sasa kwa nini unapiga kelele?

Je, huna mfalme,

Au je, mshauri wako ameangamia,

Hivi kwamba umeshikwa na uchungu kama mwanamke anayezaa?+

10 Gaagaa na kulia kwa uchungu, Ee binti ya Sayuni,

Kama mwanamke anayezaa,

Kwa maana sasa utatoka jijini na kuishi shambani.

Utaenda mpaka Babiloni,+

Na huko utaokolewa;+

Huko Yehova atakununua tena kutoka mikononi mwa maadui wako.+

11 Sasa mataifa mengi yatakusanyika dhidi yako;

Yatasema, ‘Acheni achafuliwe,

Macho yetu na yaone Sayuni likipatwa na jambo hili.’

12 Lakini hawajui mawazo ya Yehova,

Hawaelewi kusudi* lake;

Kwa maana atawakusanya kwenye uwanja wa kupuria kama safu ya miganda ya nafaka iliyotoka kukatwa.

13 Inuka upure, Ee binti ya Sayuni;+

Kwa sababu nitabadili pembe zako ziwe chuma,

Nami nitabadili kwato zako ziwe shaba,

Nawe utapondaponda kabisa mataifa mengi.+

Faida yao isiyo ya haki utamtolea Yehova,

Na mali zao utampa Bwana wa kweli wa dunia yote.”+

5 “Sasa unajikatakata,

Ee binti unayeshambuliwa;

Tumezingirwa.+

Wanampiga mwamuzi wa Israeli shavuni kwa fimbo.+

 2 Na wewe, Ee Bethlehemu Efratha,+

Uliye mdogo sana usiweze kuwa miongoni mwa maelfu ya* Yuda,+

Kutoka kwako atatoka kwa ajili yangu yule atakayekuwa mtawala katika Israeli,

Ambaye asili yake ni ya tangu nyakati za kale, tangu siku za zamani za kale.

 3 Kwa hiyo atawaacha

Mpaka wakati ambapo mwanamke anayepaswa kuzaa atakapozaa.

Na wale ndugu zake wengine watarudi kwa watu wa Israeli.

 4 Atasimama na kuchunga katika nguvu za Yehova,+

Katika ukuu wa jina la Yehova Mungu wake.

Nao watakaa kwa usalama,+

Kwa maana sasa ukuu wake utafika kwenye miisho ya dunia.+

 5 Naye ataleta amani.+

Mwashuru akiivamia nchi yetu na kukanyaga-kanyaga minara yetu yenye ngome,+

Tutawainua wachungaji saba dhidi yake, naam, wakuu* wanane wanadamu.

 6 Wataichunga nchi ya Ashuru kwa upanga,+

Na nchi ya Nimrodi+ kwenye malango yake.

Naye atatuokoa kutoka kwa Mwashuru,+

Anapoivamia nchi yetu na kulikanyaga-kanyaga eneo letu.

 7 Waliobaki wa Yakobo watakuwa miongoni mwa mataifa mengi

Kama umande kutoka kwa Yehova,

Kama manyunyu ya mvua juu ya mimea

Ambayo hayamtumaini mwanadamu

Wala kuwangojea wana wa wanadamu.

 8 Waliobaki wa Yakobo watakuwa miongoni mwa mataifa,

Miongoni mwa mataifa mengi,

Kama simba miongoni mwa wanyama wa mwituni,

Kama mwanasimba* miongoni mwa makundi ya kondoo,

Ambaye hupita na kurukia na kurarua vipandevipande;

Wala hakuna yeyote wa kuwaokoa.

 9 Mkono wako utainuliwa juu ya maadui wako,

Na maadui wako wote wataangamizwa.”

10 “Siku hiyo,” asema Yehova,

“Nitawaangamiza kabisa farasi wako na kuharibu magari yako ya vita.

11 Nitaharibu majiji yaliyo katika nchi yako

Na kubomoa ngome zako zote.

12 Nitakomesha ulozi wako,*

Na hakuna mchawi yeyote atakayebaki miongoni mwako.+

13 Nitaharibu sanamu zako za kuchongwa na nguzo zako,

Nawe hutaiinamia tena kazi ya mikono yako.+

14 Nitang’oa miti yako mitakatifu*+

Na kuharibu kabisa majiji yako.

15 Kwa hasira na ghadhabu nitalipiza kisasi

Dhidi ya mataifa ambayo hayajatii.”

6 Sikieni, tafadhali, jambo analosema Yehova.

Simameni, pelekeni kesi mbele ya milima,

Vilima na visikie sauti yenu.+

 2 Sikieni kesi ya Yehova, enyi milima,

Enyi misingi imara ya dunia,+

Kwa maana Yehova ana kesi dhidi ya watu wake;

Atateta dhidi ya Israeli:+

 3 “Watu wangu, nimewafanya nini?

Nimewachoshaje?+

Toeni ushahidi dhidi yangu.

 4 Kwa maana niliwapandisha kutoka nchini Misri,+

Kutoka katika nyumba ya utumwa niliwakomboa;+

Nilimtuma Musa, Haruni, na Miriamu mbele yenu.+

 5 Watu wangu, tafadhali, kumbukeni pendekezo la Mfalme Balaki wa Moabu,+

Na jibu ambalo Balaamu mwana wa Beori alimpa+

—Kile kilichotukia kuanzia Shitimu+ mpaka Gilgali+—

Ili mjue matendo ya uadilifu ya Yehova.”

 6 Nitakuja mbele za Yehova nikiwa na nini?

Nitainama mbele za Mungu aliye juu nikiwa na nini?

Je, nitakuja mbele zake nikiwa na dhabihu nzima za kuteketezwa,

Nikiwa na ndama wenye umri wa mwaka mmoja?+

 7 Je, Yehova atapendezwa na maelfu ya kondoo dume,

Na makumi ya maelfu ya mito ya mafuta?+

Je, nitamtoa mwanangu mzaliwa wa kwanza kwa ajili ya uasi wangu,

Uzao wa mwili wangu kwa ajili ya dhambi yangu?*+

 8 Ee mwanadamu, amekuambia yaliyo mema.

Na Yehova anataka* nini kutoka kwako?

Anataka tu utekeleze haki,*+ uthamini sana ushikamanifu,*+

Na utembee kwa kiasi+ na Mungu wako!+

 9 Sauti ya Yehova inaliita jiji;

Wale walio na hekima inayotumika wataliogopa jina lako.

Isikilizeni fimbo na yule aliyeichagua.+

10 Je, bado kuna hazina za uovu katika nyumba ya mwovu

Na kipimo kilichopunguka cha efa* kinachochukiza?

11 Je, ninaweza kuwa safi kimaadili* nikiwa na mizani ya uovu,

Nikiwa na mfuko wenye mawe ya kupimia ya udanganyifu?+

12 Kwa maana matajiri wake wamejaa ukatili,

Na wakaaji wake husema uwongo;+

Ulimi wao ni mdanganyifu kinywani mwao.+

13 “Kwa hiyo, nitakupiga na kukujeruhi,+

Na kukuacha katika hali ya ukiwa kwa sababu ya dhambi zako.

14 Utakula lakini hutashiba;

Utahisi njaa.+

Vitu utakavyotoa, hutaenda navyo kwa usalama,

Na utakavyoenda navyo, nitaviharibu kwa upanga.

15 Utapanda mbegu, lakini hutavuna.

Utakanyaga-kanyaga zeituni, lakini hutatumia mafuta yake;

Nawe utatengeneza divai mpya, lakini hutakunywa divai hata kidogo.+

16 Kwa maana unashika sheria za Omri na matendo yote ya nyumba ya Ahabu,+

Nawe unafuata ushauri wao.

Ndiyo sababu nitakufanya kuwa kitu cha kutisha

Na wakaaji wake kuwa kitu cha kupigiwa mluzi;+

Nawe utabeba dharau za mataifa.”+

7 Ole wangu! Mimi ni kama mtu ambaye,

Baada ya matunda ya kiangazi kukusanywa

Na masalio kuokotwa baada ya mavuno ya zabibu,

Hapati kishada chochote cha zabibu za kula,

Wala tini inayoiva mapema ninayotamani kula.*

 2 Mtu mshikamanifu ameangamia* duniani;

Miongoni mwa wanadamu hakuna yeyote aliye mnyoofu.+

Wote huvizia ili wamwage damu.+

Kila mmoja anamwinda ndugu yake mwenyewe kwa wavu wa kukokotwa.

 3 Mikono yao ni stadi katika kutenda maovu;+

Mkuu anadai vitu,

Hakimu anaomba zawadi,+

Mtu maarufu anasema vitu anavyotamani,*+

Nao hupanga njama pamoja.*

 4 Aliye bora zaidi kati yao ni kama miiba,

Na mnyoofu zaidi kati yao ni mbaya zaidi kuliko uzio wa miiba.

Siku ya walinzi wako na siku utakayowajibishwa itakuja.+

Sasa watashikwa na wasiwasi.+

 5 Usimwamini mwenzako

Wala usimtumaini rafiki wa karibu.+

Uwe mwangalifu kuhusu mambo unayomwambia yule unayelala ukiwa umemkumbatia.

 6 Kwa maana mwana anamdharau baba yake,

Binti anashindana na mama yake,+

Na binti mkwe anampinga mama mkwe wake;+

Maadui wa mtu ni watu wa nyumbani mwake.+

 7 Lakini mimi, nitaendelea kumtazamia Yehova.+

Nitaonyesha mtazamo wa kumngojea* Mungu wa wokovu wangu.+

Mungu wangu atanisikia.+

 8 Usishangilie juu yangu, ewe adui yangu.*

Ingawa nimeanguka, nitasimama;

Ingawa ninakaa gizani, Yehova atakuwa nuru yangu.

 9 Ghadhabu ya Yehova nitaivumilia

—Kwa maana nimemtendea dhambi—+

Mpaka atakapoitetea kesi yangu na kutekeleza haki kwa ajili yangu.

Atanileta nje kwenye nuru;

Nitautazama uadilifu wake.

10 Adui yangu pia ataona,

Na aibu itamfunika yule aliyeniambia:

“Yuko wapi Yehova Mungu wako?”+

Macho yangu yatamtazama adui yangu.

Sasa atakanyagwa-kanyagwa kama matope barabarani.

11 Itakuwa siku ya kujenga kuta zako za mawe;

Siku hiyo mipaka itapanuliwa.*

12 Siku hiyo watakuja kwako

Watatoka mbali kule Ashuru na katika majiji ya Misri,

Kutoka Misri hadi kufika Mto Efrati;

Kutoka bahari mpaka bahari na kutoka mlima mpaka mlima.+

13 Na nchi itakuwa katika hali ya ukiwa kwa sababu ya wakaaji wake,

Kwa sababu ya mambo waliyotenda.*

14 Wachunge watu wako kwa fimbo yako, kundi la urithi wako,+

Yule aliyekuwa akiishi peke yake msituni—katika shamba la matunda.

Waache wale Bashani na Gileadi+ kama ilivyokuwa siku za kale.

15 “Kama ilivyokuwa katika siku ulizotoka nchini Misri,

Nitamwonyesha yeye mambo ya ajabu.+

16 Mataifa yataona na kuaibika licha ya nguvu zote walizo nazo.+

Watafunika kinywa chao kwa mkono wao;

Masikio yao yatakuwa kiziwi.

17 Wataramba mavumbi kama nyoka;+

Kama wanyama wanaotambaa wa duniani watatoka katika ngome zao wakitetemeka.

Watakuja kwa Yehova Mungu wetu wakiwa na hofu,

Nao watakuogopa wewe.”+

18 Ni Mungu gani aliye kama wewe,

Unayesamehe dhambi na kuachilia makosa+ ya watu waliobaki wa urithi wako?+

Hutaendelea kuwa na hasira milele,

Kwa maana unapendezwa na upendo mshikamanifu.+

19 Utatuonyesha tena rehema;+ utazishinda* dhambi zetu.

Utazitupa dhambi zao zote katika vilindi vya bahari.+

20 Utamtendea Yakobo kwa uaminifu,

Na Abrahamu kwa upendo mshikamanifu,

Kama ulivyowaapia mababu zetu tangu siku za kale.+

Ufupisho wa jina Mikaeli au Mikaya linalomaanisha “Ni Nani Aliye Kama Yehova?”

Au “nchi tambarare za chini zitagawanyika.”

Tnn., “Nitayamwaga.”

Au “malipo yote ya ukahaba wake yatateketezwa motoni.”

Au “Katika nyumba ya Afra.”

Tnn., “ewe mkaaji wa kike.”

Au “za kwaheri.”

Au “mnyang’anyi.”

Tnn., “hamtauondoa kwenye shingo zenu.”

Au labda, “kutoka kwenye.”

Au “chungu cha kupikia chenye mdomo mpana.”

Au labda, “wanapokuwa na kitu cha kutafuna.”

Tnn., “wanaotakasa.”

Au “ubashiri.”

Au “watafumba vinywa vyao.”

Tnn., “Vichwa.”

Au “hubashiri.”

Au “fedha.”

Au “wanadai wanamwegemea Yehova.”

Au “mlima wa hekalu.”

Au “kilima chenye msitu.”

Au “Katika kipindi cha mwisho cha zile siku.”

Au “mafundisho yatatoka.”

Au “kurekebisha.”

Au “Wataishi.”

Au “awali.”

Au “shauri.”

Au “koo za.”

Au “viongozi.”

Au “mwanasimba mwenye manyoya marefu shingoni.”

Tnn., “kutoka mkononi mwako.”

Angalia Kamusi.

Au “dhambi ya nafsi yangu?”

Au “anadai.”

Au “uwe mwenye haki; bila upendeleo.”

Au “uwe mwenye fadhili na mshikamanifu katika upendo wako.” Tnn., “upende upendo mshikamanifu.”

Angalia Nyongeza B14.

Au “bila hatia.”

Au “ambayo nafsi yangu inatamani.”

Au “ametoweka.”

Au “tamaa ya nafsi yake.”

Tnn., “huisokota pamoja.”

Au “Nitamngojea kwa subira.”

Katika Kiebrania, neno “adui” liko katika jinsia ya kike.

Au labda, “amri itakuwa mbali sana.”

Tnn., “kwa sababu ya matokeo ya matendo yao.”

Au “utazikanyaga-kanyaga chini; utazitiisha.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki