Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt Yoeli 1:1-3:21
  • Yoeli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yoeli
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Yoeli

YOELI

1 Neno la Yehova lililomjia Yoeli* mwana wa Pethueli:

 2 “Sikilizeni jambo hili, enyi wazee,

Sikilizeni kwa makini, enyi wakaaji wote wa nchi.*

Je, jambo kama hili limewahi kutokea katika siku zenu

Au katika siku za mababu zenu?+

 3 Wasimulieni wana wenu jambo hilo,

Na acheni wana wenu wawasimulie wana wao kulihusu,

Na wana wao wasimulie kizazi kitakachofuata.

 4 Kilichoachwa na nzige wanaokula sana, kimeliwa na nzige wanaoruka katika makundi;+

Na kilichoachwa na nzige wanaoruka katika makundi, kimeliwa na tunutu;

Na kilichoachwa na tunutu, kimeliwa na parare* wanaokula sana.+

 5 Enyi walevi,+ amkeni mlie!

Pigeni mayowe, ninyi nyote mnaokunywa divai,

Kwa sababu divai tamu imeondolewa vinywani mwenu.+

 6 Kwa maana taifa limeivamia nchi yangu, lenye nguvu na lisilo na idadi.+

Meno yake ni meno ya simba,+ na mataya yake ni ya simba.

 7 Limeharibu mzabibu wangu na kuacha mtini wangu ukiwa kisiki,

Limebambua magamba yote na kuyatupa pembeni,

Na kuacha matawi yake yakiwa meupe.

 8 Ombolezeni kwa sauti kama bikira* aliyevaa nguo za magunia

Anayeomboleza kwa ajili ya bwana harusi* wa ujana wake.

 9 Toleo la nafaka+ na toleo la kinywaji+ hayapo tena kwenye nyumba ya Yehova;

Makuhani, wahudumu wa Yehova, wanaomboleza.

10 Mashamba yameharibiwa, ardhi inaomboleza;+

Kwa kuwa nafaka imeharibiwa, divai mpya imekauka, mafuta yametoweka.+

11 Wakulima wamefadhaika, watunzaji wa mizabibu wanapiga mayowe,

Kwa sababu ya ngano na shayiri;

Kwa maana mavuno ya shambani yameharibika.

12 Mzabibu umekauka,

Mtini umenyauka.

Mkomamanga, mtende, na mtofaa,

Miti yote shambani imekauka;+

Kwa maana badala ya kuwa na shangwe, watu wameshikwa na aibu.

13 Vaeni* nguo za magunia na kuomboleza,* enyi makuhani;

Pigeni mayowe, enyi wahudumu wa madhabahu.+

Ingieni na kulala hekaluni usiku kucha mkiwa mmevaa nguo za magunia, enyi wahudumu wa Mungu wangu;

Kwa maana matoleo ya nafaka+ na matoleo ya vinywaji+ hayaletwi tena katika nyumba ya Mungu wenu.

14 Tangazeni watu wafunge;* waiteni watu kwenye kusanyiko takatifu.+

Wakusanyeni wazee, pamoja na wakaaji wote wa nchi,

Kwenye nyumba ya Yehova Mungu wenu,+ nanyi mlilieni Yehova awasaidie.

15 Ole kwa sababu ya ile siku!

Kwa maana siku ya Yehova iko karibu,+

Nayo itakuja kama maangamizi kutoka kwa Mweza-Yote!

16 Je, chakula hakijaondolewa mbele ya macho yetu wenyewe,

Na shangwe na furaha kutoka katika nyumba ya Mungu wetu?

17 Mbegu* zimenyauka chini ya sepetu zao.

Maghala yamebaki ukiwa.

Maghala ya nafaka yamebomolewa, kwa maana nafaka imekauka.

18 Hata mifugo inalia kwa uchungu!

Makundi ya ng’ombe yanatangatanga huku na huku, kwa maana hayana malisho!

Na hata makundi ya kondoo yamepata adhabu.

19 Nitakuita wewe, Ee Yehova;+

Kwa maana moto umeteketeza kabisa malisho nyikani,

Na mwali wa moto umeteketeza miti yote shambani.

20 Hata wanyama wa mwituni wanasubiri kwa hamu uwasaidie,

Kwa sababu vijito vya maji vimekauka

Na moto umeteketeza kabisa malisho nyikani.”

2 “Pigeni pembe Sayuni!+

Pigeni kelele za vita katika mlima wangu mtakatifu.

Wakaaji wote wa nchi* na watetemeke,

Kwa maana siku ya Yehova inakuja!+ Iko karibu!

 2 Ni siku ya giza na utusitusi,+

Siku ya mawingu na utusitusi mzito,+

Giza hilo litaenea kama nuru ya mapambazuko juu ya milima.

Kuna taifa lenye watu wengi na lenye nguvu;+

Halijawahi kamwe kuwepo taifa kama hilo,

Na halitakuwepo tena kamwe taifa lingine kama hilo

Katika miaka yote ya vizazi vyote.

 3 Moto unateketeza kila kitu kilicho mbele yake,

Na vitu vilivyo nyuma yake vinateketezwa na mwali wa moto.+

Kabla halijapita nchi huwa kama bustani ya Edeni,+

Lakini baada ya kupita nchi inabaki nyika iliyo ukiwa,

Na hakuna chochote kinachoweza kuponyoka.

 4 Linafanana na farasi,

Nao hukimbia kama farasi wa vita.+

 5 Wanaporuka juu ya vilele vya milima, sauti yao ni kama ya magari ya vita,+

Kama sauti ya moto mkali unaoteketeza majani makavu.

Wao ni kama taifa lenye nguvu lililojipanga kivita.+

 6 Kwa sababu yao, mataifa yatakuwa na maumivu makali.

Kila uso utageuka na kuwa mwekundu kwa sababu yao.

 7 Wanashambulia kama mashujaa,

Wanapanda ukuta kama wanajeshi,

Kila mmoja wao anaendelea kufuata mwendo wake mwenyewe,

Nao hawatoki katika njia zao.

 8 Hawasukumani;

Kila mtu hupiga mwendo kwenye njia yake.

Baadhi yao wakiuawa kwa silaha,

Wengine hawavunji safu zao.

 9 Wanaingia haraka jijini, nao hukimbia ukutani.

Hupanda juu ya nyumba, na kuingia kama mwizi madirishani.

10 Nchi inatetemeka mbele yao na mbingu kutikisika.

Jua na mwezi vimekuwa na giza,+

Na nyota zimepoteza mwangaza wake.

11 Yehova atapaza sauti mbele ya jeshi lake,+ kwa maana jeshi lake ni kubwa sana.+

Kwa maana anayetekeleza neno Lake ni mwenye nguvu;

Kwa maana siku ya Yehova ni kuu na inaogopesha sana.+

Ni nani anayeweza kuistahimili?”+

12 “Hata sasa,” asema Yehova, “rudini kwangu kwa mioyo yenu yote,+

Kwa kufunga+ na kulia na kuomboleza.

13 Irarueni mioyo yenu,+ wala si mavazi yenu,+

Nanyi mrudi kwa Yehova Mungu wenu,

Kwa maana ni mwenye huruma* na rehema, si mwepesi wa hasira,+ naye ana upendo mwingi mshikamanifu,+

Naye atafikiria upya* msiba aliokusudia kuleta.

14 Ni nani ajuaye ikiwa hatabadili nia na kuufikiria upya*+

Na kuwaachia baraka,

Ili mweze kumtolea Yehova Mungu wenu toleo la nafaka na toleo la kinywaji?

15 Pigeni pembe Sayuni!

Tangazeni watu wafunge;* waiteni watu kwenye kusanyiko takatifu.+

16 Wakusanyeni watu; litakaseni kutaniko.+

Wakusanyeni wanaume wazee;* wakusanyeni watoto wadogo na pia watoto wanaonyonya.+

Bwana harusi na atoke katika chumba chake cha ndani, na bibi harusi atoke katika chumba chake cha bibi harusi.

17 Kati ya ukumbi na madhabahu+

Acheni makuhani, wahudumu wa Yehova, walie na kusema:

‘Ee Yehova, wahurumie watu wako;

Usifanye urithi wako uwe kitu cha kudharauliwa,

Kwa kuacha mataifa yawatawale.

Kwa nini mataifa yaseme: “Yuko wapi Mungu wao?”’+

18 Kwa hiyo Yehova atakuwa na bidii kwa ajili ya nchi yake

Na kuwahurumia watu wake.+

19 Yehova atawajibu hivi watu wake:

‘Tazama, ninawaletea nafaka na divai mpya na mafuta,

Nanyi mtatosheka kabisa;+

Sitafanya tena mshutumiwe miongoni mwa mataifa.+

20 Nitamfukuza mbali nanyi mkaaji wa kaskazini;

Nitamtawanya katika nchi kavu iliyo ukiwa,

Walinzi wake wa mbele kuelekea bahari ya mashariki*

Na walinzi wake wa nyuma kuelekea bahari ya magharibi.*

Na harufu yake mbaya itapanda juu,

Na uvundo wake utaendelea kupanda juu;+

Kwa maana Atafanya mambo makuu.’

21 Usiogope, Ee nchi.

Uwe na shangwe na furaha, kwa maana Yehova atafanya mambo makuu.

22 Msiogope, enyi wanyama wa mwituni,

Kwa maana malisho ya nyikani yatakuwa kijani kibichi,+

Na miti itazaa matunda;+

Mitini na mizabibu itazaa kwa wingi.*+

23 Enyi wana wa Sayuni, iweni na shangwe na kumshangilia Yehova Mungu wenu;+

Kwa maana atawapa kiasi kinachofaa cha mvua ya vuli,

Naye atawaletea mvua kubwa,

Mvua ya vuli na mvua ya masika, kama ilivyokuwa awali.+

24 Viwanja vya kupuria vitajaa nafaka safi,

Na mashinikizo yatafurika divai mpya na mafuta.+

25 Nami nitafidia miaka ambayo

Mazao yenu yaliliwa na nzige wanaoruka katika makundi, tunutu, parare wanaokula sana, na nzige* wanaokula sana,

Jeshi langu kubwa ambalo nililituma miongoni mwenu.+

26 Kwa hakika mtakula na kutosheka,+

Nanyi mtalisifu jina la Yehova Mungu wenu,+

Ambaye ametenda mambo yenye kustaajabisha kwa niaba yenu;

Watu wangu hawataaibishwa tena kamwe.+

27 Nanyi mtalazimika kujua kwamba nimo miongoni mwa Waisraeli+

Na kwamba mimi ni Yehova Mungu wenu+—hakuna mwingine!

Watu wangu hawataaibishwa tena kamwe.

28 Kisha nitaimimina roho yangu+ juu ya kila aina ya mwili,

Na wana wenu na mabinti wenu watatoa unabii,

Na wanaume wenu wazee wataota ndoto,

Na wanaume wenu vijana wataona maono.+

29 Na hata juu ya watumwa wangu wa kiume na watumwa wa kike

Nitaimimina roho yangu siku hizo.

30 Nami nitafanya mambo ya ajabu* mbinguni na duniani,

Damu na moto na nguzo za moshi.+

31 Jua litatiwa giza na mwezi utatiwa damu+

Kabla ya kuja kwa ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha.+

32 Na kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa;+

Kwa maana kwenye Mlima Sayuni na katika Yerusalemu kutakuwa na wale wanaosalimika,+ kama Yehova alivyosema,

Waokokaji wanaoitwa na Yehova.”

3 “Kwa maana tazama! katika siku hizo na wakati huo,

Nitakapowarudisha mateka wa Yuda na Yerusalemu,+

 2 Nitakusanya pia mataifa yote

Na kuyaleta chini kwenye Bonde la* Yehoshafati.*

Na humo nitawahukumu+

Kwa ajili ya watu wangu na urithi wangu Israeli,

Kwa maana waliwatawanya miongoni mwa mataifa,

Nao waligawana nchi yangu miongoni mwao.+

 3 Nao waligawana watu wangu kwa kura;+

Walimuuza mvulana ili wamlipe kahaba

Na kumuuza msichana ili wanunue divai wanywe.

 4 Pia, kwa nini mnanitendea hivi,

Enyi watu wa Tiro na Sidoni na maeneo yote ya Ufilisti?

Je, mnanilipiza kisasi kwa sababu ya jambo fulani?

Ikiwa mnanilipiza kisasi,

Nitawalipiza kisasi haraka, naam, upesi.*+

 5 Kwa sababu mmechukua fedha na dhahabu yangu,+

Nanyi mmepeleka hazina zangu bora kabisa kwenye mahekalu yenu;

 6 Na watu wa Yuda na Yerusalemu mmewauza kwa Wagiriki,+

Mkawaondoa na kuwapeleka mbali na eneo lao;

 7 Tazameni, nitawachochea watoke mahali mlipowauza,+

Nami nitawalipiza kisasi.*

 8 Nitawauza wana wenu na mabinti wenu kwa watu wa Yuda,+

Nao watawauza kwa wanaume wa Sheba, kwa taifa lililo mbali sana;

Kwa maana Yehova mwenyewe amesema hilo.

 9 Tangazeni hili miongoni mwa mataifa:+

‘Jitayarisheni kwa ajili ya* vita! Wachocheeni wanaume hodari!

Wanajeshi wote na wakaribie, acheni wapige mwendo!+

10 Yafueni majembe yenu yawe mapanga na miundu yenu iwe mikuki.

Aliye dhaifu na aseme: “Nina nguvu.”

11 Njooni msaidie, enyi mataifa yote jirani, kusanyikeni pamoja!’”+

Ee Yehova, wateremshe mahali hapo wenye nguvu* wako.

12 “Mataifa na yachochewe na kuja kwenye Bonde la* Yehoshafati;

Kwa maana nitaketi huko ili kuyahukumu mataifa yote jirani.+

13 Tieni mundu, kwa maana mavuno yamekomaa.

Teremkeni na kuyakanyaga, kwa maana shinikizo la divai limejaa.+

Mitungi inafurika, kwa sababu uovu wao ni mwingi.

14 Umati, umati umo katika bonde la* uamuzi,

Kwa maana siku ya Yehova iko karibu katika bonde la* uamuzi.+

15 Jua na mwezi vitakuwa giza,

Na nyota zitapoteza mwangaza wake.

16 Na Yehova atanguruma kutoka Sayuni,

Atapaza sauti yake kutoka Yerusalemu.

Na mbingu na dunia zitatikisika;

Lakini Yehova atakuwa kimbilio kwa watu wake,+

Ngome kwa watu wa Israeli.

17 Nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova Mungu wenu, ninayekaa Sayuni, mlima wangu mtakatifu.+

Yerusalemu litakuwa mahali patakatifu,+

Na wageni hawatapita tena humo.+

18 Siku hiyo milima itadondosha divai tamu,+

Vilima vitatiririka maziwa,

Na vijito vyote vya Yuda vitatiririka maji.

Kutoka katika nyumba ya Yehova kijito kitatiririka,+

Nacho kitanywesha Bonde la* Miti ya Mishita.

19 Lakini Misri itakuwa ukiwa,+

Na Edomu itakuwa nyika iliyo ukiwa,+

Kwa sababu ya ukatili waliowatendea watu wa Yuda,+

Katika nchi yao walimwaga damu isiyo na hatia.+

20 Lakini Yuda itakaliwa daima,

Na Yerusalemu kizazi baada ya kizazi.+

21 Damu yao niliyoiona kuwa na hatia nitaiona kuwa isiyo na hatia;+

Na Yehova atakaa Sayuni.”+

Maana yake “Yehova Ni Mungu.”

Au “dunia.”

Au “panzi.”

Au “mwanamwali.”

Au “mume.”

Tnn., “Jifungeni.”

Tnn., “kujipiga vifua.”

Tnn., “Takaseni mfungo.”

Au labda, “Tini zilizokaushwa.”

Au “dunia.”

Au “neema.”

Au “ataghairi kuhusu.”

Au “kughairi.”

Tnn., “Takaseni mfungo.”

Au “wazee.”

Yaani, Bahari ya Chumvi.

Yaani, Bahari ya Mediterania.

Tnn., “kikamili.”

Au “panzi.”

Au “miujiza.”

Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”

Maana yake “Yehova Ni Mwamuzi.”

Tnn., “Nitaleta kisasi haraka, upesi juu ya vichwa vyenu.”

Tnn., “Nitaleta kisasi juu ya vichwa vyenu.”

Tnn., “Takaseni.”

Au “mashujaa.”

Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”

Au “nchi tambarare ya chini ya.”

Au “nchi tambarare ya chini ya.”

Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki