KWA WAGALATIA
1 Paulo, mtume, si kutokana na wanadamu wala kupitia mwanadamu, bali kupitia Yesu Kristo+ na Mungu Baba,+ aliyemfufua kutoka kwa wafu, 2 na ndugu wote walio pamoja nami, kwa makutaniko ya Galatia:
3 Na muwe na fadhili zisizostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo. 4 Alijitoa mwenyewe kwa ajili ya dhambi zetu+ ili atuokoe kutoka katika mfumo huu mwovu wa mambo,*+ kulingana na mapenzi ya Mungu na Baba yetu,+ 5 na awe na utukufu milele na milele. Amina.
6 Ninashangaa kwamba mnageuzwa* upesi kutoka kwa Yule aliyewaita kwa fadhili zisizostahiliwa za Kristo nanyi mnaenda kwenye habari njema ya aina nyingine.+ 7 Si kwamba kuna habari njema nyingine; lakini kuna watu fulani wanaowataabisha ninyi+ na kutaka kupotosha habari njema kuhusu Kristo. 8 Hata hivyo, ikiwa sisi au malaika kutoka mbinguni tungewatangazia kuwa habari njema jambo tofauti na habari njema tuliyowatangazia, mtu huyo na alaaniwe. 9 Kama tulivyosema awali, sasa ninasema tena, Yeyote anayewatangazia kuwa habari njema jambo tofauti na lile mlilopokea, na alaaniwe.
10 Kwa kweli, je, sasa ninajaribu kuwashawishi wanadamu au Mungu? Au je, ninajaribu kuwapendeza wanadamu? Kama bado ningekuwa ninawapendeza wanadamu, singekuwa mtumwa wa Kristo. 11 Akina ndugu, ningependa mjue kwamba habari njema niliyowatangazia haitokani na wanadamu;+ 12 kwa kuwa sikuipokea kutoka kwa mwanadamu, wala sikufundishwa, bali ilikuwa kupitia ufunuo wa Yesu Kristo.
13 Bila shaka, mlisikia kuhusu mwenendo wangu wa zamani katika dini ya Kiyahudi,+ kwamba niliendelea kulitesa sana* kutaniko la Mungu na kuliangamiza;+ 14 nami nilikuwa nikifanya maendeleo makubwa katika dini ya Kiyahudi kuliko watu wengi wa umri wangu katika taifa langu, kwa maana nilikuwa na bidii zaidi kwa ajili ya mapokeo ya baba zangu.+ 15 Lakini Mungu, aliyenitenga tangu tumbo la uzazi la mama yangu na kuniita kupitia fadhili zake zisizostahiliwa,+ alipoona vema 16 kumfunua Mwana wake kupitia kwangu, ili niyatangazie mataifa habari njema kumhusu,+ sikushauriana papo hapo na mwanadamu yeyote;* 17 wala sikupanda kwenda Yerusalemu kwa wale waliokuwa mitume kabla yangu, bali nilienda Arabia, kisha nikarudi Damasko.+
18 Miaka mitatu baadaye, nilipanda kwenda Yerusalemu+ kumtembelea Kefa,*+ nami nikakaa pamoja naye siku 15. 19 Lakini sikuwaona wale mitume wengine, isipokuwa Yakobo+ ndugu ya Bwana. 20 Basi kuhusu mambo ninayowaandikia, ninawahakikishia mbele za Mungu kwamba sisemi uwongo.
21 Baada ya hapo nikaenda katika maeneo ya Siria na Kilikia.+ 22 Lakini mimi binafsi sikujulikana kwa makutaniko ya Yudea yaliyokuwa katika muungano na Kristo. 23 Walikuwa tu wakisikia: “Yule mtu ambaye alitutesa+ hapo zamani sasa anatangaza habari njema kuhusu imani ambayo hapo zamani aliiangamiza.”+ 24 Basi wakaanza kumtukuza Mungu kwa sababu yangu.
2 Baada ya miaka 14 nilipanda tena kwenda Yerusalemu pamoja na Barnaba,+ na Tito pia.+ 2 Lakini nilienda kutokana na ufunuo, nami nikawajulisha habari njema ambayo ninahubiri kati ya mataifa. Hata hivyo, nilifanya hivyo faraghani, mbele ya wanaume walioheshimiwa sana, ili kuhakikisha kwamba sikuwa ninakimbia bure au sikuwa nimekimbia bure. 3 Hata hivyo, hata Tito,+ aliyekuwa pamoja nami, hakulazimishwa kutahiriwa,+ ingawa alikuwa Mgiriki. 4 Lakini jambo hilo lilitokea kwa sababu ya akina ndugu wa uwongo walioingizwa kimyakimya,+ walioingia kisirisiri ili kupeleleza uhuru+ tunaofurahia katika muungano na Kristo Yesu, ili watufanye kuwa watumwa kabisa;+ 5 hatukukubaliana nao wala kujitiisha kwao,+ hapana, hata kwa muda mfupi,* ili kweli ya habari njema iendelee kuwa pamoja nanyi.
6 Lakini kuhusu wale walioonekana kuwa muhimu+—vyovyote walivyokuwa hapo awali sioni tofauti, kwa maana Mungu haangalii sura ya nje—watu hao walioheshimiwa sana hawakuniongezea kitu chochote kipya. 7 Badala yake, walipoona kwamba nilikuwa nimekabidhiwa habari njema kwa ajili ya wale wasiotahiriwa,+ kama vile Petro alivyokabidhiwa kwa ajili ya wale waliotahiriwa— 8 kwa maana yule aliyemtia Petro nguvu kwa ajili ya utume kwa wale waliotahiriwa, alinitia nguvu mimi pia kwa ajili ya watu wa mataifa+— 9 nao walipotambua fadhili zisizostahiliwa nilizopewa,+ Yakobo+ na Kefa* na Yohana, ambao walionekana kuwa nguzo, walinipa mimi na Barnaba+ mkono wa kulia wa kushirikiana,* ili sisi twende kwa mataifa, nao waende kwa watu waliotahiriwa. 10 Walituomba tuwakumbuke maskini, nami nimejitahidi sana kufanya jambo hilo.+
11 Hata hivyo, Kefa*+ alipokuja Antiokia,+ nilimpinga* uso kwa uso, kwa sababu kwa hakika alikuwa amekosea.* 12 Kwa maana kabla ya watu fulani kutoka kwa Yakobo+ kufika, alikuwa akila chakula pamoja na watu wa mataifa;+ lakini walipofika, akaacha kufanya hivyo, akajitenga kwa kuwaogopa wale waliotahiriwa.+ 13 Wayahudi wengine pia wakajiunga naye katika unafiki huo, hivi kwamba hata wakamshawishi Barnaba katika unafiki wao. 14 Lakini nilipoona kwamba hawakuwa wakitembea kwa unyoofu kulingana na kweli ya habari njema,+ nilimwambia Kefa* mbele yao wote: “Ikiwa wewe, ingawa ni Myahudi unaishi kama mataifa wanavyoishi, na si kama Wayahudi wanavyoishi, unawezaje kuwalazimisha watu wa mataifa waishi kulingana na mazoea ya Kiyahudi?”+
15 Sisi tulio Wayahudi kwa kuzaliwa, na si watenda dhambi kutoka kwa mataifa, 16 tunatambua kwamba mtu hutangazwa kuwa mwadilifu, si kupitia matendo ya sheria, bali kupitia tu imani+ katika Yesu Kristo.+ Basi sisi tumeweka imani yetu katika Kristo Yesu, ili tutangazwe kuwa waadilifu kupitia imani katika Kristo bali si kupitia matendo ya sheria, kwa maana hakuna mtu yeyote atakayetangazwa* kuwa mwadilifu kupitia matendo ya sheria.+ 17 Sasa ikiwa sisi pia tumepatikana kuwa watenda dhambi tulipokuwa tukitafuta kutangazwa kuwa waadilifu kupitia Kristo, basi je, Kristo ni mhudumu wa dhambi? La hasha! 18 Ikiwa ninayajenga tena mambo ambayo wakati mmoja niliyabomoa, ninaonyesha kwamba mimi ni mkosaji. 19 Kwa maana kupitia sheria nilikufa kuielekea sheria,+ ili niwe hai kumwelekea Mungu. 20 Mimi nimetundikwa mtini pamoja na Kristo.+ Si mimi tena niliye hai,+ bali ni Kristo anayeishi katika muungano na mimi. Kwa kweli, uhai ninaoishi sasa katika mwili ninaishi kwa imani katika Mwana wa Mungu,+ aliyenipenda na kujitoa mwenyewe kwa ajili yangu.+ 21 Mimi sizikatai* fadhili zisizostahiliwa za Mungu,+ kwa maana ikiwa uadilifu ni kupitia sheria, kwa kweli Kristo alikufa bure.+
3 Enyi Wagalatia wasio na akili! Ni nani aliyewaleta chini ya uvutano huu mwovu,+ ninyi mliofafanuliwa waziwazi jinsi Yesu Kristo alivyotundikwa mtini?+ 2 Ninataka kuwauliza* jambo hili moja: Je, mlipokea roho kupitia matendo ya sheria au kwa sababu ya kuamini mambo mliyosikia?+ 3 Je, ninyi hamna akili kabisa? Baada ya kuanza mwendo wa kiroho,* je, mnamalizia katika mwendo wa kimwili?*+ 4 Je, mlipatwa na mateso mengi sana bila sababu? Ikiwa kwa kweli ilikuwa bila sababu. 5 Kwa hiyo, je, yule anayewapa ninyi roho na kufanya matendo yenye nguvu+ kati yenu, anayafanya kwa sababu ya matendo ya sheria au kwa sababu mnaamini mambo mliyosikia? 6 Kama vile Abrahamu “alivyokuwa na imani katika Yehova,* na ikahesabiwa kwake kuwa ni uadilifu.”+
7 Bila shaka mnajua kwamba wale wanaoshikamana na imani ni wana wa Abrahamu.+ 8 Kwa hiyo, andiko likitangulia kuona kwamba Mungu atawatangaza watu wa mataifa kuwa waadilifu kupitia imani, lilitangaza habari njema mwanzoni kwa Abrahamu, yaani: “Kupitia kwako mataifa yote yatabarikiwa.”+ 9 Basi wale wanaoshikamana na imani wanabarikiwa pamoja na Abrahamu, aliyekuwa na imani.+
10 Wote wanaotegemea matendo ya sheria wako chini ya laana, kwa maana imeandikwa: “Amelaaniwa kila mtu asiyedumu katika mambo yote yaliyoandikwa katika kitabu cha kukunjwa cha Sheria kwa kuyatenda.”+ 11 Isitoshe, ni wazi kwamba kupitia sheria hakuna mtu atakayetangazwa kuwa mwadilifu mbele za Mungu,+ kwa maana “mwadilifu ataishi kupitia imani.”+ 12 Sasa Sheria haitegemei imani. Badala yake, “yeyote anayefanya mambo hayo ataishi kupitia mambo hayo.”+ 13 Kristo alitununua,+ akatuweka huru+ kutoka katika laana ya Sheria akawa laana badala yetu, kwa sababu imeandikwa: “Amelaaniwa kila mtu aliyetundikwa kwenye mti.”+ 14 Ilikuwa hivyo ili baraka ya Abrahamu ije kwa mataifa kupitia Kristo Yesu,+ ili tuipokee roho iliyoahidiwa+ kupitia imani yetu.
15 Akina ndugu, ninazungumza kwa kutumia mfano wa mwanadamu: Agano linapohalalishwa, hata kama ni kupitia mwanadamu, hakuna mtu anayelifuta au kuliongezea jambo lolote. 16 Sasa ahadi zilitolewa kwa Abrahamu na kwa uzao wake.*+ Haisemi, “na kwa wazao wako,”* kana kwamba ni wengi. Badala yake, inasema, “na kwa uzao wako,”* kana kwamba ni kwa mmoja, ambaye ni Kristo.+ 17 Isitoshe, ninasema hivi: Sheria iliyotokezwa miaka 430 baadaye,+ haivunji agano lililofanywa na Mungu mwanzoni, na haifuti ahadi. 18 Kwa maana ikiwa urithi unategemea sheria, hautegemei tena ahadi; lakini Mungu amempa Abrahamu urithi kwa fadhili kupitia ahadi.+
19 Basi, kwa nini Sheria? Iliongezwa ili kufanya makosa yawe wazi,+ mpaka ufike ule uzao*+ ambao ulikuwa umepewa ahadi; na ilipitishwa kupitia malaika+ kwa mkono wa mpatanishi.+ 20 Sasa hakuna mpatanishi wakati mtu mmoja tu ndiye anayehusika, lakini Mungu ni mmoja tu. 21 Kwa hiyo, je, Sheria inapinga ahadi za Mungu? La hasha! Kwa maana ikiwa kungekuwa na sheria inayoweza kuleta uhai, kwa kweli uadilifu ungekuwa kupitia sheria. 22 Lakini Andiko liliyafunga mambo yote katika kifungo cha dhambi, ili ahadi inayotokana na imani katika Yesu Kristo ipewe wale wanaoamini.*
23 Hata hivyo, kabla ya imani kufika, tulikuwa tukilindwa chini ya sheria, tukiwekwa kifungoni, tukiitazamia imani iliyokusudiwa kufunuliwa.+ 24 Basi Sheria imekuwa mtunzaji* wetu ikituongoza kwa Kristo,+ ili tutangazwe kuwa waadilifu kupitia imani.+ 25 Lakini sasa kwa kuwa imani imefika,+ hatuko tena chini ya mtunzaji.*+
26 Kwa kweli, ninyi nyote ni wana wa Mungu+ kupitia imani yenu katika Kristo Yesu.+ 27 Kwa maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo.+ 28 Hakuna Myahudi wala Mgiriki,+ hakuna mtumwa wala mtu huru,+ hakuna mwanamume wala mwanamke,+ kwa maana ninyi nyote ni kitu kimoja katika muungano na Kristo Yesu.+ 29 Isitoshe, ikiwa ninyi ni wa Kristo, ninyi kwa kweli ni uzao wa* Abrahamu,+ warithi+ kuhusiana na ahadi.+
4 Basi ninasema kwamba mrithi akiwa bado mtoto mdogo, hayuko tofauti na mtumwa, ingawa ndiye bwana wa vitu vyote, 2 bali yuko chini ya watunzaji na wasimamizi mpaka siku iliyopangwa mapema na baba yake. 3 Vivyo hivyo, sisi pia tulipokuwa watoto, tulikuwa watumwa wa mambo ya msingi ya ulimwengu.+ 4 Lakini wakati kamili ulipofika, Mungu alimtuma Mwana wake, aliyezaliwa na mwanamke+ na pia alikuwa chini ya sheria,+ 5 ili awaachilie huru kwa kuwanunua wale walio chini ya sheria,+ ili sisi tufanywe kuwa wana.+
6 Sasa kwa sababu ninyi ni wana, Mungu ametuma roho+ ya Mwana wake ndani ya mioyo yetu,+ nayo hupaza sauti: “Abba,* Baba!”+ 7 Kwa hiyo, wewe si mtumwa tena bali ni mwana; na ikiwa ni mwana, basi wewe pia ni mrithi kupitia Mungu.+
8 Hata hivyo, wakati hamkumjua Mungu, mlikuwa watumwa wa miungu ya uwongo.* 9 Lakini sasa kwa kuwa mmemjua Mungu au, kwamba sasa Mungu amewajua ninyi, kwa nini mnarudi tena kwenye mambo ya msingi yaliyo dhaifu+ na yasiyo na maana na kutaka kuyatumikia tena?+ 10 Mnashika kwa uangalifu sana siku na miezi+ na majira na miaka. 11 Ninaogopa kwa ajili yenu, isiwe kwamba nimepoteza jitihada zangu kwenu.
12 Ninawaomba akina ndugu, iweni kama nilivyo, kwa sababu mimi pia nilikuwa kama mlivyo.+ Hamkunikosea. 13 Lakini mnajua ni kwa sababu ya ugonjwa wa kimwili kwamba nilipata nafasi yangu ya kwanza ya kuwatangazia habari njema. 14 Na ingawa hali yangu ya kimwili ilikuwa jaribu kwenu, hamkunitendea kwa dharau au kunichukia;* bali mlinipokea kama malaika wa Mungu, kama Kristo Yesu. 15 Furaha mliyokuwa nayo iko wapi? Kwa maana ninawatolea ushahidi kwamba, kama ingewezekana, mngeyang’oa macho yenu na kunipa.+ 16 Hivyo basi, je, nimekuwa adui yenu kwa sababu ninawaambia ukweli? 17 Wanawatafuta kwa bidii ili muwafuate, bali si kwa kusudi zuri; wanataka kuwatenganisha nami, ili muwafuate wao kwa bidii. 18 Hata hivyo, ni vema sikuzote kwa mtu kuwatafuta ninyi kwa bidii kwa kusudi zuri bali si wakati tu ninapokuwa pamoja nanyi, 19 watoto wangu wadogo,+ ambao tena nina uchungu wa kuwazaa mpaka Kristo atakapofanyizwa* ndani yenu. 20 Ninatamani ningekuwa pamoja nanyi sasa hivi na kuzungumza kwa njia tofauti, kwa sababu ninawahangaikia ninyi.
21 Niambieni, ninyi mnaotaka kuwa chini ya sheria, Je, hamsikii Sheria? 22 Kwa mfano, imeandikwa kwamba Abrahamu alikuwa na wana wawili, mmoja kupitia kijakazi+ na mwingine kupitia mwanamke aliye huru;+ 23 lakini yule wa kijakazi kwa kweli alizaliwa kupitia njia ya asili*+ na yule mwingine wa mwanamke aliye huru kupitia ahadi.+ 24 Mambo haya yanaweza kumaanisha tukio la mfano; kwa maana wanawake hawa wanamaanisha maagano mawili, moja kutoka Mlima Sinai,+ ambalo huzaa watoto kwa ajili ya utumwa na ambalo ni Hagari. 25 Basi Hagari anamaanisha Sinai,+ mlima ulio Arabia, naye analingana na Yerusalemu la leo, kwa maana liko katika utumwa pamoja na watoto wake. 26 Lakini Yerusalemu la juu liko huru, nalo ni mama yetu.
27 Kwa maana imeandikwa: “Furahi, wewe mwanamke tasa usiyezaa; piga vigelegele vya shangwe, wewe mwanamke usiye na uchungu wa kuzaa; kwa maana watoto wa mwanamke aliye ukiwa ni wengi kuliko wa yule aliye na mume.”+ 28 Basi, akina ndugu, ninyi ni watoto wa ahadi kama Isaka alivyokuwa.+ 29 Lakini kama ilivyokuwa wakati huo, yule aliyezaliwa kupitia njia ya asili* alianza kumtesa yule aliyezaliwa kupitia roho,+ ndivyo ilivyo pia sasa.+ 30 Hata hivyo, andiko linasema nini? “Mfukuze kijakazi na mwanawe, kwa maana mwana wa kijakazi hatakuwa mrithi kamwe pamoja na mwana wa mwanamke aliye huru.”+ 31 Basi, akina ndugu, sisi si watoto wa kijakazi, bali wa yule mwanamke aliye huru.
5 Kristo alituweka huru ili tuwe na uhuru kama huo. Kwa hiyo, simameni imara,+ na msijiache mfungwe tena katika nira ya utumwa.+
2 Oneni! Mimi, Paulo, ninawaambia kwamba mkitahiriwa, Kristo hatakuwa na faida kwenu.+ 3 Tena ninatoa ushahidi kwa kila mtu anayetahiriwa kwamba yuko chini ya wajibu wa kuitimiza Sheria yote.+ 4 Mmetenganishwa na Kristo, ninyi mnaojaribu kutangazwa kuwa waadilifu kupitia sheria;+ mmeanguka kutoka kwenye fadhili zake zisizostahiliwa. 5 Kwa upande wetu, kupitia kwa roho tunasubiri kwa hamu uadilifu uliotumainiwa unaotokana na imani. 6 Kwa maana katika muungano na Kristo Yesu, kutahiriwa au kutotahiriwa hakuna faida yoyote,+ bali imani inayotenda kupitia upendo ina faida.
7 Mlikuwa mnakimbia vema.+ Ni nani aliyewazuia kuendelea kuitii kweli? 8 Ushawishi wa namna hii hautoki kwa Yule anayewaita ninyi. 9 Chachu kidogo huchachisha donge zima.+ 10 Nina uhakika kwamba ninyi mlio katika muungano na Bwana+ hamtakuja kufikiria jambo tofauti; lakini yule anayewasababishia taabu,+ hata iwe ni nani, atapokea hukumu anayostahili. 11 Na mimi, akina ndugu, ikiwa bado ninahubiri kuhusu kutahiriwa, kwa nini bado ninateswa? Ikiwa ndivyo, kikwazo cha mti wa mateso*+ kimeondolewa. 12 Ningependa watu wanaojaribu kuwaangusha ninyi wajihasi wenyewe.*
13 Akina ndugu, mliitwa kwenye uhuru; lakini msiutumie uhuru huo kama nafasi ya kufuatilia tamaa za mwili,+ bali mtumikiane kupitia upendo.+ 14 Kwa maana Sheria nzima imetimizwa* katika amri hii moja: “Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.”+ 15 Lakini, ikiwa mnaendelea kuumana na kuraruana,+ jihadharini ili msije mkaangamizana.+
16 Lakini ninasema, Endeleeni kutembea kwa roho+ nanyi hamtatenda kwa tamaa za mwili hata kidogo.+ 17 Kwa maana mwili katika tamaa yake unapingana na roho, na roho inapingana na mwili; vitu hivyo vinapingana, hivi kwamba hamfanyi mambo mnayotaka kufanya.+ 18 Isitoshe, ikiwa mnaongozwa na roho, ninyi hamko chini ya sheria.
19 Sasa matendo ya mwili huonekana wazi, nayo ni uasherati,*+ uchafu, mwenendo mpotovu,*+ 20 ibada ya sanamu, kuwasiliana na roho,*+ chuki, mizozo, wivu, milipuko ya hasira, migogoro, migawanyiko, madhehebu, 21 husuda, ulevi,+ karamu zenye vurugu, * na mambo kama hayo.+ Ninawaonya mapema kuhusu mambo hayo, kama vile nilivyowaonya tayari, kwamba wale wanaozoea kufanya mambo hayo hawataurithi Ufalme wa Mungu.+
22 Kwa upande mwingine, tunda la roho* ni upendo, shangwe, amani, subira,* fadhili, wema,+ imani, 23 upole, kujizuia.*+ Hakuna sheria dhidi ya mambo hayo. 24 Isitoshe, wale walio wa Kristo Yesu wametundika mwili mtini pamoja na mawazo na tamaa zake mbaya.+
25 Ikiwa tunaishi kwa roho, na tuendelee pia kutembea kwa utaratibu kwa roho.+ 26 Tusiwe tukijisifu,+ tusichochee mashindano kati yetu,+ wala tusioneane wivu.
6 Akina ndugu, hata mtu akichukua hatua isiyofaa kabla hajajua, ninyi mlio na sifa za kustahili kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu huyo kwa roho ya upole.+ Lakini kila mmoja wenu aendelee kujiangalia,+ kwa kuwa ninyi pia mnaweza kujaribiwa.+ 2 Endeleeni kubebeana mizigo mizito,+ na hivyo mtaitimiza sheria ya Kristo.+ 3 Kwa maana mtu akifikiri yeye ni kitu wakati yeye si kitu,+ anajidanganya mwenyewe. 4 Lakini kila mmoja na achunguze matendo yake mwenyewe,+ kisha atakuwa na sababu ya kushangilia kuhusiana na yeye mwenyewe, na si kwa kujilinganisha na mtu mwingine.+ 5 Kwa maana kila mtu ataubeba mzigo* wake mwenyewe.+
6 Zaidi ya hayo, mtu yeyote anayefundishwa* neno na ashiriki katika mambo yote mema pamoja na yule anayetoa fundisho hilo.*+
7 Msipotoshwe: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia;+ 8 kwa sababu yule anayepanda kwa mwili wake atavuna uharibifu kutokana na mwili wake, lakini yule anayepanda kwa roho, atavuna uzima wa milele kutokana na roho.+ 9 Basi tusife moyo katika kufanya mema, kwa maana kwa wakati unaofaa tutavuna ikiwa hatutachoka kabisa.*+ 10 Basi, tukiwa bado na nafasi,* acheni tuwatendee watu wote mema, na hasa wale ambao ni ndugu zetu katika imani.
11 Oneni kwamba nimewaandikia kwa herufi kubwa kwa mkono wangu mwenyewe.
12 Wote wanaotaka kujionyesha kuwa wazuri katika mwili* ndio wanaojaribu kuwalazimisha mtahiriwe, wakifanya hivyo ili tu wasiteswe kwa ajili ya mti wa mateso* wa Kristo. 13 Kwa maana hata wale wanaotahiriwa hawaishiki Sheria,+ lakini wanataka mtahiriwe ili wawe na sababu ya kujisifu kuhusu mwili wenu. 14 Lakini sitajisifu kamwe, isipokuwa katika mti wa mateso* wa Bwana wetu Yesu Kristo,+ ambaye kupitia kwake ulimwengu umeuawa* kuhusiana nami, nami kuhusiana na ulimwengu. 15 Kwa maana kutahiriwa si kitu wala kutotahiriwa,+ bali kiumbe kipya ndicho kitu.+ 16 Na wale wote wanaotembea kwa utaratibu kwa kanuni hii ya mwenendo, juu yao na kuwe na amani na rehema, ndiyo, juu ya Israeli wa Mungu.+
17 Kuanzia sasa mtu yeyote asinitaabishe, kwa maana ninabeba mwilini mwangu alama za mtumwa wa Yesu.+
18 Akina ndugu, fadhili zisizostahiliwa za Bwana wetu Yesu Kristo ziwe pamoja na roho mnayoonyesha. Amina.
Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Au “mnaondolewa.”
Tnn., “mpaka hatua inayozidi mno.”
Tnn., “na mwili na damu.”
Pia anaitwa Petro.
Tnn., “kwa saa moja.”
Pia anaitwa Petro.
Au “ushirikiano.”
Pia anaitwa Petro.
Au “nilimkabili.”
Au “alikuwa na hatia.”
Pia anaitwa Petro.
Tnn., “mwili utakaotangazwa.”
Au “sizitupi.”
Tnn., “kujifunza kutoka kwenu.”
Tnn., “kuanza katika roho.”
Tnn., “mnakamilishwa katika mwili.”
Angalia Nyongeza A5.
Tnn., “mbegu yake.”
Tnn., “mbegu zako.”
Tnn., “mbegu yako.”
Tnn., “ile mbegu.”
Au “wanaoonyesha imani.”
Au “mfundishaji; mlezi.”
Au “mfundishaji; mlezi.”
Tnn., “mbegu ya.”
Neno la Kiebrania au Kiaramu linalomaanisha “Ee Baba!”
Tnn., “ ile ambayo kwa kweli si miungu.”
Au “kunitemea mate.”
Au “atakapoumbwa.”
Tnn., “kulingana na mwili.”
Tnn., “kulingana na mwili.”
Angalia Kamusi.
Au “wawe matowashi,” na hivyo wasistahili kufuata sheria ambayo walikuwa wakiitetea.
Au labda, “imejumlishwa.”
Neno la Kigiriki porneiʹa. Angalia Kamusi.
Au “ufidhuli; matendo ya kuchukiza yanayofanywa bila aibu.” Kigiriki, a·selʹgei·a. Angalia Kamusi.
Au “uchawi.”
Au “karamu za kupindukia.”
Au “sifa zinazotokezwa na roho.”
Au “ustahimilivu.”
Au “kujidhibiti; kujiweza.”
Au “mzigo wa wajibu.”
Au “anayefundishwa kwa mdomo.”
Au “fundisho hilo la mdomo.”
Au “hatutakufa moyo.”
Tnn., “wakati unaofaa.”
Au “wanaotaka kuonekana wazuri kwa nje.”
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Au “umeuawa kwenye mti.”