BARUA YA KWANZA YA YOHANA
1 Kile kilichokuwapo tangu mwanzo, tulichokisikia na kukiona kwa macho yetu, ambacho tumekitazama na mikono yetu ikakigusa, kuhusiana na neno la uzima,+ 2 (ndiyo, uzima ulifunuliwa, nasi tumeona na tunatoa ushahidi+ na kuwajulisha kuhusu uzima wa milele+ ambao Baba alikuwa nao, na uliofunuliwa kwetu), 3 kile ambacho tumeona na kusikia tunawajulisha pia,+ ili ninyi vilevile muwe na ushirika pamoja nasi. Na huu ushirika wetu ni pamoja na Baba na pamoja na Mwana wake Yesu Kristo.+ 4 Nasi tunaandika mambo haya ili shangwe yetu iwe kamili.
5 Huu ndio ujumbe tuliosikia kutoka kwake nasi tunawatangazia ninyi: Mungu ni nuru,+ na hakuna giza kamwe ndani yake.* 6 Ikiwa tunasema, “Tuna ushirika pamoja naye,” na bado tunaendelea kutembea katika giza, tunasema uwongo nasi hatuishi kulingana na kweli.+ 7 Hata hivyo, ikiwa tunatembea katika nuru kama yeye mwenyewe alivyo katika nuru, tuna ushirika sisi kwa sisi, na damu ya Yesu Mwana wake hutusafisha kutoka katika dhambi yote.+
8 Ikiwa tunasema, “Hatuna dhambi,” tunajipotosha wenyewe+ na kweli haimo ndani yetu. 9 Tukiungama dhambi zetu, yeye ni mwaminifu na mwadilifu naye atatusamehe dhambi zetu na kutusafisha ukosefu wote wa uadilifu.+ 10 Ikiwa tunasema, “Hatujatenda dhambi,” tunamfanya yeye kuwa mwongo, na neno lake halimo ndani yetu.
2 Watoto wangu wadogo, ninawaandikia mambo haya ili msitende dhambi. Na bado, yeyote akitenda dhambi, tuna msaidizi* kwa Baba, Yesu Kristo,+ mtu mwadilifu.+ 2 Naye ni dhabihu ya upatanisho*+ kwa ajili ya dhambi zetu,+ lakini si kwa ajili ya dhambi zetu tu bali pia dhambi za ulimwengu wote.+ 3 Na kwa jambo hili tunatambua kwamba tumemjua yeye, yaani, tukiendelea kuzishika amri zake. 4 Mtu anayesema, “Mimi nimemjua,” na bado hashiki amri zake ni mwongo, na kweli haimo ndani ya mtu huyo. 5 Lakini yeyote anayeshika neno lake, kwa kweli upendo wa Mungu umekamilishwa katika mtu huyo.+ Hivyo ndivyo tunajua kwamba sisi tumo katika muungano na yeye.+ 6 Mtu anayesema kwamba anakaa katika muungano na yeye, ana wajibu wa kuendelea kutembea kama huyo alivyotembea.+
7 Wapendwa, siwaandikii amri mpya, bali amri ya zamani ambayo mmekuwa nayo tangu mwanzo.+ Amri hiyo ya zamani ni neno ambalo mlisikia. 8 Tena, ninawaandikia amri mpya, ambayo ni ya kweli kumhusu yeye na kuwahusu ninyi, kwa sababu giza linapitilia mbali na nuru ya kweli tayari inaangaza.+
9 Mtu anayesema kwamba yumo katika nuru na bado anamchukia+ ndugu yake bado yumo katika giza.+ 10 Mtu anayempenda ndugu yake hukaa katika nuru,+ naye hana kikwazo chochote. 11 Lakini mtu anayemchukia ndugu yake yumo katika giza na anatembea katika giza,+ naye hajui anakoenda,+ kwa sababu giza limeyapofusha macho yake.
12 Ninawaandikia ninyi watoto wadogo, kwa sababu mmesamehewa dhambi zenu kwa ajili ya jina lake.+ 13 Ninawaandikia ninyi akina baba, kwa sababu mmemjua yule aliye wa tangu mwanzo. Ninawaandikia ninyi vijana, kwa sababu mmemshinda yule mwovu.+ Ninawaandikia ninyi watoto wadogo, kwa sababu mmemjua Baba.+ 14 Ninawaandikia ninyi akina baba, kwa sababu mmemjua yule aliye wa tangu mwanzo. Ninawaandikia ninyi vijana, kwa sababu mna nguvu+ na neno la Mungu hukaa ndani yenu+ nanyi mmemshinda yule mwovu.+
15 Msiupende ulimwengu au vitu vilivyo katika ulimwengu.+ Yeyote akiupenda ulimwengu, kumpenda Baba hakumo ndani yake;+ 16 kwa sababu kila kitu katika ulimwengu—tamaa ya mwili+ na tamaa ya macho+ na mtu kujionyesha mali zake maishani*—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu. 17 Zaidi ya hayo, ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake,+ lakini yule anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.+
18 Watoto wadogo, ni saa ya mwisho, na kama vile mlivyosikia kwamba mpinga-Kristo anakuja,+ hata sasa wapinga-Kristo wengi wametokea,+ na kwa sababu hiyo tunajua kwamba ni saa ya mwisho. 19 Waliondoka miongoni mwetu, lakini hawakuwa wa namna yetu;*+ kwa maana kama wangekuwa wa namna yetu, wangebaki pamoja nasi. Lakini waliondoka ili ionekane kwamba si wote walio wa namna yetu.+ 20 Nanyi mmetiwa mafuta kutoka kwa yule mtakatifu,+ na nyote mna ujuzi. 21 Ninawaandikia, si kwa sababu hamwijui kweli,+ bali kwa sababu mnaijua, na kwa sababu hakuna uwongo unaotokana na kweli.+
22 Ni nani aliye mwongo kama si yule anayekana kwamba Yesu ndiye Kristo?+ Huyo ndiye mpinga-Kristo,+ yule anayemkana Baba na Mwana. 23 Kila mtu anayemkana Mwana hana Baba pia.+ Bali yeyote anayemkiri Mwana+ ana Baba pia.+ 24 Lakini mambo mliyosikia tangu mwanzo yanapaswa kukaa ndani yenu.+ Ikiwa mambo mliyosikia tangu mwanzo yanakaa ndani yenu, ninyi pia mtakaa katika muungano na Mwana na katika muungano na Baba. 25 Zaidi ya hayo, hili ndilo jambo alilotuahidi yeye mwenyewe, uzima wa milele.+
26 Ninawaandikia mambo haya kuhusu wale wanaojaribu kuwapotosha ninyi. 27 Kutiwa mafuta ambako mlipokea kutoka kwake+ hukaa ndani yenu, na hamhitaji kufundishwa na yeyote; lakini kutiwa mafuta kutoka kwake kunawafundisha kuhusu mambo yote,+ na ni kweli si uwongo. Kama kulivyowafundisha ninyi, kaeni katika muungano na yeye.+ 28 Basi sasa, watoto wadogo, kaeni katika muungano na yeye, ili atakapofunuliwa tuwe na uhuru wa kusema+ bali tusiaibike wakati wa kuwapo kwake. 29 Ikiwa mnajua yeye ni mwadilifu, mnajua pia kwamba kila mtu aliye na mazoea ya kufanya uadilifu amezaliwa kutokana naye.+
3 Oneni upendo ambao Baba ametuonyesha,+ kwamba tunapaswa kuitwa watoto wa Mungu!+ Na hivyo ndivyo tulivyo. Ndiyo sababu ulimwengu hautujui,+ kwa sababu haumjui yeye.+ 2 Wapendwa, sasa sisi ni watoto wa Mungu,+ lakini bado haijafunuliwa jinsi tutakavyokuwa.+ Tunajua kwamba atakapofunuliwa tutakuwa kama yeye, kwa sababu tutamwona kama alivyo. 3 Na kila mtu aliye na tumaini hili ndani yake hujisafisha,+ kama huyo alivyo safi.
4 Kila mtu aliye na mazoea ya kufanya dhambi anaendelea pia kufanya uasi sheria, na dhambi ni uasi sheria. 5 Mnajua pia kwamba alifunuliwa ili kuondoa dhambi zetu,+ na hakuna dhambi ndani yake. 6 Kila mtu anayekaa katika muungano na yeye hana mazoea ya kufanya dhambi;+ mtu yeyote aliye na mazoea ya kufanya dhambi hajamwona wala kumjua. 7 Watoto wadogo, yeyote asiwapotoshe; mtu anayeendelea kufanya uadilifu ni mwadilifu, kama huyo alivyo mwadilifu. 8 Mtu aliye na mazoea ya kufanya dhambi hutokana na Ibilisi, kwa sababu Ibilisi amekuwa akifanya dhambi tangu mwanzo.*+ Kwa kusudi hili Mwana wa Mungu alifunuliwa, ili avunje* kazi za Ibilisi.+
9 Kila mtu ambaye amezaliwa kutokana na Mungu haendelei kufanya dhambi,+ kwa sababu mbegu* Yake hukaa ndani ya mtu huyo, naye hawezi kuendelea kufanya dhambi, kwa sababu amezaliwa kutokana na Mungu.+ 10 Watoto wa Mungu na watoto wa Ibilisi ni wazi kwa jambo hili: Yeyote ambaye haendelei kufanya uadilifu hatokani na Mungu, wala yule ambaye hampendi ndugu yake.+ 11 Kwa maana huu ndio ujumbe ambao mmesikia tangu mwanzo, kwamba tunapaswa kupendana;+ 12 si kama Kaini, aliyetokana na yule mwovu akamuua ndugu yake. Na kwa nini alimuua?+ Kwa sababu matendo yake mwenyewe yalikuwa maovu,+ lakini matendo ya ndugu yake yalikuwa ya uadilifu.+
13 Akina ndugu, msishangae kwamba ulimwengu unawachukia.+ 14 Tunajua kwamba tumevuka kutoka kifo mpaka uzima,+ kwa sababu tunawapenda akina ndugu.+ Mtu ambaye hapendi hukaa katika kifo.+ 15 Kila mtu anayemchukia ndugu yake ni muuaji,+ nanyi mnajua kwamba hakuna muuaji aliye na uzima wa milele ndani yake.+ 16 Sisi tumeujua upendo, kwa sababu huyo alitoa uhai wake* kwa ajili yetu,+ nasi tuna wajibu wa kutoa uhai wetu* kwa ajili ya ndugu zetu.+ 17 Lakini yeyote aliye na mali za ulimwengu huu akimwona ndugu yake akiwa na uhitaji naye akatae kumhurumia, anawezaje kuwa na upendo wa Mungu ndani yake?+ 18 Watoto wadogo, tunapaswa kupendana, si kwa neno au kwa ulimi,+ bali kwa tendo+ na kweli.+
19 Kwa jambo hili tutajua kwamba tunatokana na kweli, nasi tutaihakikishia* mioyo yetu mbele zake 20 kuhusu jambo lolote ambalo huenda mioyo yetu ikatuhukumu, kwa sababu Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.+ 21 Wapendwa, ikiwa mioyo yetu haituhukumu, tuna uhuru wa kusema na Mungu;+ 22 na chochote tunachoomba tunapokea kutoka kwake,+ kwa sababu tunazishika amri zake na tunafanya mambo yanayopendeza machoni pake. 23 Kwa kweli, hii ndiyo amri yake: kwamba tuwe na imani katika jina la Mwana wake Yesu Kristo+ na tupendane,+ kama vile alivyotupatia amri. 24 Zaidi ya hayo, mtu anayeshika amri zake hukaa katika muungano na yeye, na yeye katika muungano na mtu huyo.+ Na kupitia roho aliyotupatia, tunajua kwamba anakaa katika muungano pamoja nasi.+
4 Wapendwa, msiamini kila neno lililoongozwa na roho,*+ lakini yajaribuni maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatoka kwa Mungu,+ kwa kuwa manabii wengi wa uwongo wameingia ulimwenguni.+
2 Hivi ndivyo mnavyojua ikiwa neno lililoongozwa na roho limetoka kwa Mungu: Kila neno lililoongozwa na roho linalokiri kwamba Yesu Kristo alikuja katika mwili linatoka kwa Mungu.+ 3 Lakini kila neno lililoongozwa na roho ambalo halimkiri Yesu halitoki kwa Mungu.+ Zaidi ya hayo, hili ndilo neno lililoongozwa na roho la yule mpinga-Kristo ambalo mmesikia kwamba linakuja,+ na sasa tayari limo ulimwenguni.+
4 Ninyi mnatokana na Mungu, watoto wadogo, nanyi mmewashinda,+ kwa sababu yule aliye katika muungano na ninyi+ ni mkuu kuliko yule aliye katika muungano na ulimwengu.+ 5 Wao hutokana na ulimwengu;+ ndiyo sababu wanasema mambo yanayotokana na ulimwengu na ulimwengu huwasikiliza.+ 6 Sisi tunatokana na Mungu. Yeyote anayemjua Mungu hutusikiliza;+ yeyote ambaye hatokani na Mungu hatusikilizi.+ Hivi ndivyo tunavyolitofautisha neno la kweli lililoongozwa na roho na neno lenye kosa lililoongozwa na roho.+
7 Wapendwa, na tuendelee kupendana,+ kwa sababu upendo unatoka kwa Mungu, na kila mtu ambaye hupenda amezaliwa kutokana na Mungu na anamjua Mungu.+ 8 Yeyote ambaye hapendi hajamjua Mungu, kwa sababu Mungu ni upendo.+ 9 Hivi ndivyo upendo wa Mungu ulivyofunuliwa kwetu, kwamba Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee+ ulimwenguni ili tupate uzima kupitia yeye.+ 10 Hivi ndivyo upendo ulivyo, si kwamba sisi tumempenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda akamtuma Mwana wake kuwa dhabihu ya upatanisho*+ kwa ajili ya dhambi zetu.+
11 Wapendwa, ikiwa Mungu alitupenda hivi, basi sisi pia tuna wajibu wa kupendana.+ 12 Hakuna mtu ambaye amemwona Mungu wakati wowote.+ Tukiendelea kupendana, Mungu hukaa ndani yetu na upendo wake unakamilishwa ndani yetu.+ 13 Hivi ndivyo tunavyojua kwamba tunakaa katika muungano na yeye na yeye katika muungano na sisi, kwa sababu ametupatia roho yake. 14 Isitoshe, sisi wenyewe tumemwona na tunatoa ushahidi kwamba Baba amemtuma Mwana wake kuwa mwokozi wa ulimwengu.+ 15 Yeyote anayekiri kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu,+ Mungu hukaa katika muungano na mtu huyo na yeye katika muungano na Mungu.+ 16 Nasi tumejua na tumeamini kwamba Mungu anatupenda.+
Mungu ni upendo,+ na mtu anayekaa katika upendo hukaa katika muungano na Mungu, na Mungu hukaa katika muungano na yeye.+ 17 Kwa njia hii upendo umekamilishwa ndani yetu, ili tuwe na uhuru wa kusema*+ katika siku ya hukumu, kwa sababu, kama huyo alivyo, ndivyo tulivyo katika ulimwengu huu. 18 Hakuna woga katika upendo,+ lakini upendo mkamilifu hutupa* woga nje, kwa sababu woga hutuzuia. Kwa kweli, mtu aliye mwoga hajakamilishwa katika upendo.+ 19 Sisi tuna upendo, kwa sababu alitupenda kwanza.+
20 Yeyote akisema, “Ninampenda Mungu,” na bado anamchukia ndugu yake, yeye ni mwongo.+ Kwa maana mtu ambaye hampendi ndugu yake,+ ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hajamwona.+ 21 Nasi tuna amri hii kutoka kwake, kwamba yeyote anayempenda Mungu lazima pia ampende ndugu yake.+
5 Kila mtu anayeamini kwamba Yesu ndiye Kristo amezaliwa kutokana na Mungu,+ na kila mtu anayempenda yule aliyesababisha kuzaliwa humpenda yule ambaye amezaliwa kutokana na huyo. 2 Hivi ndivyo tunavyojua kwamba tunawapenda watoto wa Mungu,+ kwa kumpenda Mungu na kushika amri zake. 3 Kwa maana kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake;+ na bado amri zake si mzigo mzito,+ 4 kwa sababu kila mtu aliyezaliwa* kutokana na Mungu huushinda ulimwengu.+ Na huu ndio ushindi ambao umeushinda ulimwengu, imani yetu.+
5 Ni nani anayeweza kuushinda ulimwengu?+ Ni yule anayeamini kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu.+ 6 Huyu ndiye aliyekuja kupitia maji na damu, Yesu Kristo, si kwa maji tu,+ bali kwa maji na kwa damu.+ Na roho inatoa ushahidi,+ kwa sababu roho ndiyo kweli. 7 Kwa maana kuna vitu vitatu vinavyotoa ushahidi: 8 roho+ na maji+ na damu;+ na hivyo vitatu vinakubaliana.
9 Tukikubali ushahidi wa wanadamu, ushahidi wa Mungu ni mkuu zaidi. Kwa sababu huu ndio ushahidi ambao Mungu hutoa, ushahidi ambao ametoa kumhusu Mwana wake. 10 Mtu anayemwamini Mwana wa Mungu, ana ushahidi ndani yake. Mtu asiyemwamini Mungu amemfanya yeye kuwa mwongo,+ kwa sababu hana imani katika ushahidi uliotolewa na Mungu kumhusu Mwana wake. 11 Na huu ndio ushahidi, kwamba Mungu alitupatia uzima wa milele,+ na uzima huu umo ndani ya Mwana wake.+ 12 Mtu aliye na Mwana ana uzima huu; mtu ambaye hana Mwana wa Mungu hana uzima huu.+
13 Ninawaandikia mambo haya ili ninyi mlio na imani katika jina la Mwana wa Mungu+ mjue kwamba mna uzima wa milele.+ 14 Na huu ndio uhakika tulio nao kwake,+ kwamba tukiomba chochote kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.+ 15 Na ikiwa tunajua kwamba anatusikia kuhusiana na chochote tunachoomba, tunajua kwamba tutapata mambo tuliyomwomba, kwa kuwa tumeyaomba kwake.+
16 Yeyote akimwona ndugu yake akifanya dhambi isiyoleta kifo, yeye ataomba, na Mungu atampa huyo uzima,+ ndiyo, kwa wale ambao hawafanyi dhambi inayoleta kifo. Kuna dhambi ambayo huleta kifo.+ Simwambii aombe kuhusu dhambi hiyo. 17 Ukosefu wote wa uadilifu ni dhambi,+ na bado kuna dhambi isiyoleta kifo.
18 Tunajua kwamba kila mtu aliyezaliwa kutokana na Mungu hana mazoea ya kufanya dhambi, lakini yeye hulindwa na yule aliyezaliwa kutokana na Mungu,* na yule mwovu hawezi kumshika.*+ 19 Tunajua tunatokana na Mungu, lakini ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.+ 20 Hata hivyo, tunajua kwamba Mwana wa Mungu amekuja,+ naye ametupatia ufahamu* ili tuweze kumjua yule aliye wa kweli. Nasi tumo katika muungano na yule aliye wa kweli,+ kupitia Mwana wake, Yesu Kristo. Huyo ndiye Mungu wa kweli na uzima wa milele.+ 21 Watoto wadogo, jiepusheni na sanamu.+
Au “katika muungano naye.”
Au “wakili.”
Au “dhabihu ya kufunika dhambi; njia ya kuleta maelewano.”
Au “mtu kujigamba kuhusu mali zake.”
Au “hawakuwa wenzetu.”
Au “tangu alipoanza.”
Au “aangamize.”
Yaani, mbegu inayoweza kuzaa, au inayotokeza matunda.
Au “nafsi yake.”
Au “nafsi zetu.”
Au “tutaishawishi; tutaisadikisha.”
Tnn., “kila roho.”
Au “dhabihu kwa ajili ya kufunika; njia ya kuleta maelewano.”
Au “tuwe na uhakika.”
Au “husukuma.”
Tnn., “kila kitu kilichozaliwa.”
Yaani, Yesu Kristo, Mwana wa Mungu.
Au “hamshiki imara.”
Tnn., “uwezo wa kufikiri; uwezo wa akili.”