Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt Yakobo 1:1-5:20
  • Yakobo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yakobo
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Yakobo

BARUA YA YAKOBO

1 Yakobo,+ mtumwa wa Mungu na wa Bwana Yesu Kristo, kwa yale makabila 12 yaliyotawanyika sehemu mbalimbali:

Salamu!

2 Oneni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mnapopata majaribu mbalimbali,+ 3 mkijua kwamba sifa iliyojaribiwa ya imani yenu hutokeza uvumilivu.+ 4 Lakini acheni uvumilivu ukamilishe kazi yake, ili muwe kamili na timamu katika mambo yote, bila kukosa kitu chochote.+

5 Kwa hiyo, ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu,+ kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu,*+ naye atapewa.+ 6 Lakini na aendelee kuomba kwa imani,+ bila kuwa na shaka hata kidogo,+ kwa maana aliye na shaka ni kama wimbi la bahari linaloendeshwa na upepo na kupeperushwa huku na huku. 7 Kwa kweli, mtu huyo asitarajie kupokea kitu chochote kutoka kwa Yehova;* 8 yeye ni mtu anayesitasita,+ asiye imara katika njia zake zote.

9 Lakini ndugu wa hali ya chini na ashangilie katika* kuinuliwa kwake,+ 10 naye tajiri katika kushushwa kwake,+ kwa sababu atapitilia mbali kama ua la shambani. 11 Kwa maana kama jua linavyochomoza pamoja na joto lake linalounguza na kufanya mmea unyauke, na ua lake lianguke na kuharibu urembo wake wa nje, vivyo hivyo pia, tajiri atanyauka katika mambo anayofuatilia.+

12 Mwenye furaha ni yule anayeendelea kuvumilia jaribu,+ kwa sababu atakapokubaliwa atapokea taji la uzima,+ ambalo Yehova* aliwaahidi wale wanaoendelea kumpenda.+ 13 Mtu akiwa chini ya jaribu, asiseme: “Mungu ananijaribu.” Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote. 14 Lakini kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa* na tamaa yake mwenyewe.+ 15 Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi; nayo dhambi, baada ya kufanywa, huleta kifo.+

16 Msipotoshwe, ndugu zangu wapendwa. 17 Kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu hutoka juu,+ hushuka kutoka kwa Baba wa mianga ya mbinguni,+ ambaye habadiliki au kugeuka kama kivuli.*+ 18 Yalikuwa mapenzi yake kutuzaa sisi kwa neno la kweli,+ ili kwa njia fulani tuwe matunda ya kwanza ya viumbe wake.+

19 Jueni hili, ndugu zangu wapendwa: Kila mtu lazima awe mwepesi wa kusikia, si mwepesi wa kusema,+ si mwepesi wa hasira,+ 20 kwa maana hasira ya mwanadamu haitokezi uadilifu wa Mungu.+ 21 Kwa hiyo, ondoeni uchafu wote na ubaya wote,*+ na pokeeni kwa upole kupandwa kwa lile neno linaloweza kuwaokoa.*

22 Hata hivyo, iweni watendaji wa neno,+ na si wasikiaji tu, mkijidanganya wenyewe kwa mawazo ya uwongo. 23 Kwa maana ikiwa yeyote ni msikiaji wa neno, na si mtendaji,+ huyo ni kama mtu anayeutazama uso wake* katika kioo. 24 Kwa maana yeye hujitazama na kwenda zake na kusahau mara moja jinsi alivyo. 25 Lakini anayechunguza sheria kamilifu+ ambayo ni ya uhuru na kudumu katika hiyo, amekuwa, si msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi; naye atafurahia kile anachofanya.+

26 Ikiwa mtu yeyote anafikiri yeye ni mwabudu wa Mungu* lakini haudhibiti* kabisa ulimi wake,+ anaudanganya moyo wake, na ibada yake ni ubatili. 27 Namna ya ibada* iliyo safi na isiyo na unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kuwatunza mayatima+ na wajane+ katika dhiki yao,+ na kuendelea kujitunza bila doa kutokana na ulimwengu.+

2 Ndugu zangu, je, mnashika imani ya Bwana wetu mtukufu Yesu Kristo huku mkiwa na upendeleo?+ 2 Kwa maana, ikiwa mtu aliyevaa pete za dhahabu kwenye vidole vyake na aliyevaa mavazi ya kifahari anaingia katika mkutano wenu, na mtu maskini aliyevaa mavazi yenye uchafu anaingia pia, 3 je, mnamtazama kwa kibali yule aliyevaa mavazi ya kifahari na kumwambia: “Wewe kalia kiti hiki kilicho mahali pazuri,” na kumwambia yule maskini: “Wewe simama tu,” au, “Kalia kile kiti pale chini ya kiti changu cha miguu”?+ 4 Ikiwa ndivyo ilivyo, je, hamna tofauti za kitabaka kati yenu wenyewe+ na je, hamjawa waamuzi wanaotoa maamuzi maovu?+

5 Sikilizeni, ndugu zangu wapendwa. Je, Mungu hakuwachagua walio maskini kwa maoni ya ulimwengu ili wawe matajiri katika imani+ na warithi wa Ufalme, aliowaahidi wale wanaompenda?+ 6 Lakini ninyi mmemvunjia heshima maskini. Je, si matajiri wanaowakandamiza ninyi+ na kuwakokota wakiwapeleka mahakamani? 7 Je, hawalikufuru lile jina zuri ambalo kwa hilo mliitwa? 8 Basi, ikiwa mnaifuata ile sheria ya kifalme kulingana na andiko, “Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe,”+ mnafanya vema. 9 Lakini mkiendelea kuonyesha upendeleo,+ mnafanya dhambi, na sheria inawahukumu* kuwa wakosaji.+

10 Kwa maana ikiwa yeyote anatii Sheria yote lakini anajikwaa katika jambo moja, amekosa kuitii Sheria yote.+ 11 Kwa maana yule aliyesema, “Usifanye uzinzi,”+ alisema pia: “Usiue.”+ Basi, ikiwa hufanyi uzinzi lakini unaua, umeivunja sheria. 12 Endeleeni kusema na kutenda kama wale watakaohukumiwa kwa sheria ya watu huru.*+ 13 Kwa maana yule asiye na mazoea ya kuonyesha rehema atahukumiwa bila rehema.+ Rehema hushinda hukumu.

14 Kuna faida gani, ndugu zangu, mtu fulani akisema ana imani lakini hana matendo?+ Je, imani hiyo inaweza kumwokoa?+ 15 Ikiwa ndugu au dada hawana nguo* na chakula cha kutosha kwa ajili ya siku, 16 na mmoja wenu awaambie, “Nendeni kwa amani; mwote moto na mle vizuri,” lakini bila kuwapatia mahitaji ya mwili wao, kuna faida gani?+ 17 Vivyo hivyo pia, imani bila matendo imekufa.+

18 Hata hivyo, mtu fulani atasema: “Wewe una imani, nami nina matendo. Nionyeshe imani yako bila matendo, nami nitakuonyesha imani yangu kwa matendo yangu.” 19 Wewe unaamini kuna Mungu mmoja, sivyo? Unafanya vema. Hata hivyo, roho waovu pia wanaamini na kutetemeka.+ 20 Lakini je, unataka kujua, ewe mwanadamu usiye na akili, kwamba imani bila matendo haifai kitu? 21 Je, Abrahamu baba yetu hakutangazwa kuwa mwadilifu kwa matendo baada ya kumtoa Isaka mwana wake juu ya madhabahu?+ 22 Mnaona kwamba imani yake ilitenda pamoja na matendo yake na imani yake ilikamilishwa kwa matendo yake,+ 23 na andiko likatimizwa linalosema: “Abrahamu alikuwa na imani katika Yehova,* na ikahesabiwa kwake kuwa uadilifu,”+ naye akaitwa rafiki ya Yehova.*+

24 Mnaona kwamba mtu hutangazwa kuwa mwadilifu kwa matendo, na si kwa imani peke yake. 25 Vivyo hivyo, je, Rahabu yule kahaba hakutangazwa pia kuwa mwadilifu kwa matendo, baada ya kuwakaribisha wale wajumbe na kuwatoa nje kupitia njia nyingine?+ 26 Kwa kweli, kama vile mwili bila roho* umekufa,+ vivyo hivyo, imani bila matendo imekufa.+

3 Ndugu zangu, si wengi kati yenu wanaopaswa kuwa walimu mkijua kwamba tutapokea hukumu nzito* zaidi.+ 2 Kwa maana sisi sote hujikwaa* mara nyingi.+ Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu, anayeweza kuuongoza kwa lijamu mwili wake wote pia. 3 Tunapoweka lijamu katika vinywa vya farasi ili watutii, sisi huuongoza mwili wao wote pia. 4 Tazameni hata meli: Ingawa ni kubwa sana nazo huendeshwa na upepo mkali, zinaongozwa na mtambo wa usukani ulio mdogo sana ili kwenda popote ambapo mtu aliye kwenye usukani anataka.

5 Vivyo hivyo pia, ulimi ni kiungo kidogo cha mwili na bado hujigamba sana. Tazameni jinsi moto mdogo unavyoweza kuteketeza msitu mkubwa! 6 Ulimi pia ni moto.+ Kati ya viungo vya mwili wetu, ulimi unawakilisha ulimwengu wa ukosefu wa uadilifu, kwa maana unautia mwili wote+ unajisi na kuwasha moto maisha yote* nao huwashwa moto na Gehena.* 7 Kwa maana kila aina ya mnyama wa mwituni, ndege, mnyama anayetambaa, na kiumbe wa baharini anaweza kufugwa na wamefugwa na wanadamu. 8 Lakini hakuna mwanadamu anayeweza kuufuga ulimi. Ulimi ni kitu kitundu chenye kudhuru, kilichojaa sumu yenye kuua.+ 9 Kwa ulimi tunamsifu Yehova,* aliye Baba, na bado kwa ulimi tunawalaani wanadamu ambao wameumbwa “kwa mfano wa Mungu.”+ 10 Baraka na laana hutoka katika kinywa kilekile.

Ndugu zangu, haifai mambo yatendeke hivyo.+ 11 Je, chemchemi inaweza kutoa katika shimo lilelile maji matamu* na pia machungu? 12 Ndugu zangu, je, mtini unaweza kuzaa zeituni au mzabibu kuzaa tini?+ Maji ya chumvi hayawezi kutokeza maji matamu.*

13 Ni nani mwenye hekima na uelewaji kati yenu? Na aonyeshe kwa mwenendo wake mzuri matendo yanayofanywa kwa upole unaotokana na hekima. 14 Lakini ikiwa mna wivu mkali+ na ugomvi*+ mioyoni mwenu, msiwe mkijigamba+ na kusema uwongo kuhusu ile kweli. 15 Hii siyo hekima inayoshuka kutoka juu; bali ni ya kidunia,+ ya kinyama, na ya roho waovu. 16 Kwa maana palipo na wivu na ugomvi,* pana machafuko pia na kila jambo baya.+

17 Lakini hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi,+ kisha yenye kufanya amani,+ yenye usawaziko,+ tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema,+ haina ubaguzi,+ na si ya kinafiki.+ 18 Zaidi ya hayo, tunda la uadilifu hupandwa katika hali zenye amani+ kwa* wale wanaofanya amani.+

4 Ni nini chanzo cha vita na mapigano miongoni mwenu? Je, havitokani na tamaa zenu za mwili zinazoendeleza pambano ndani yenu?*+ 2 Mnatamani, lakini hamna kitu. Mnaendelea kuua na kutamani kwa wivu, na bado hamwezi kupata. Mnaendelea kupigana na kufanya vita.+ Hamna kitu kwa sababu hamwombi. 3 Mnapoomba, hampokei kwa sababu mnaomba kwa kusudi baya, ili mvitumie kwa ajili ya tamaa zenu za mwili.

4 Enyi wazinzi,* je, hamjui kwamba urafiki na ulimwengu ni uadui na Mungu? Kwa hiyo, yeyote anayetaka kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya kuwa adui ya Mungu.+ 5 Au je, mnafikiri kwamba andiko linasema hivi bila sababu: “Roho ambayo imekaa ndani yetu huendelea kutamani kwa wivu”?+ 6 Hata hivyo, fadhili zisizostahiliwa ambazo Yeye hutoa ni kubwa zaidi. Kwa hiyo, linasema: “Mungu huwapinga wenye majivuno,+ lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.”+

7 Basi, jitiisheni kwa Mungu;+ lakini mpingeni Ibilisi,+ naye atawakimbia ninyi.+ 8 Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.+ Safisheni mikono yenu, ninyi watenda dhambi,+ na takaseni mioyo yenu,+ ninyi mnaositasita. 9 Iweni na taabu na mwomboleze na kulia.+ Kicheko chenu na kigeuzwe kuwa maombolezo, na badala ya kuwa na shangwe mkate tamaa. 10 Jinyenyekezeni machoni pa Yehova,*+ naye atawainua.+

11 Akina ndugu acheni kusemana kati yenu.+ Yeyote anayemsema vibaya ndugu au anayemhukumu ndugu yake husema vibaya juu ya sheria na kuihukumu sheria. Na ikiwa unaihukumu sheria, basi wewe si mtendaji wa sheria, bali ni mwamuzi. 12 Kuna mmoja tu ambaye ni Mpaji-sheria na Mwamuzi,+ yule anayeweza kuokoa na kuangamiza.+ Lakini wewe ni nani ili umhukumu jirani yako?+

13 Haya, basi, ninyi mnaosema: “Leo au kesho tutasafiri kwenda jiji fulani nasi tutakaa mwaka mmoja huko, tutafanya biashara na kupata faida,”+ 14 ingawa hamjui jinsi maisha yenu yatakavyokuwa kesho.+ Kwa maana ninyi ni ukungu unaotokea kwa muda kidogo na kisha kutoweka.+ 15 Badala yake, mnapaswa kusema: “Yehova* akipenda,+ tutaishi na kufanya hili au lile.” 16 Lakini sasa mnajivuna na kujigamba kwa kiburi. Majivuno yote ya namna hiyo ni maovu. 17 Kwa hiyo, ikiwa mtu anajua jinsi ya kufanya yaliyo sawa na bado hayafanyi, hiyo ni dhambi kwake.+

5 Haya basi, enyi matajiri, lieni na kupiga mayowe kwa sababu ya taabu zitakazowapata.+ 2 Utajiri wenu umeoza, na mavazi yenu yameliwa na nondo.*+ 3 Dhahabu na fedha zenu zimeliwa na kutu, na kutu hiyo itakuwa ushahidi dhidi yenu nayo itakula miili yenu. Vitu mlivyoweka akiba vitakuwa kama moto katika siku za mwisho.+ 4 Tazama! Mishahara ambayo hamjawalipa wafanyakazi waliovuna mashamba yenu, inaendelea kupaza kilio, na vilio vya kuomba msaada vya wavunaji vimefika masikioni mwa Yehova* wa majeshi.+ 5 Ninyi mmeishi kwa anasa na kwa ajili ya kutosheleza tamaa zenu duniani. Mmeinonesha mioyo yenu katika siku ya machinjo.+ 6 Mmemhukumu; mmemuua mwadilifu. Je, yeye hawapingi ninyi?

7 Basi, iweni na subira, akina ndugu, mpaka kuwapo kwa Bwana.+ Tazama! Mkulima huendelea kungojea matunda yenye thamani ya nchi, akiyasubiri mpaka mvua ya mapema na mvua ya baadaye inyeshe.+ 8 Ninyi pia iweni na subira;+ imarisheni mioyo yenu, kwa sababu kuwapo kwa Bwana kumekaribia.+

9 Msinung’unikiane,* akina ndugu, ili msihukumiwe.+ Tazama! Mwamuzi amesimama mbele ya milango. 10 Akina ndugu, fuateni mfano wa manabii waliopatwa na uovu+ na kuonyesha subira+ na ambao walisema katika jina la Yehova.*+ 11 Tazama! Tunawaona wale ambao wamevumilia kuwa wenye furaha.*+ Mmesikia kuhusu uvumilivu wa Ayubu+ na mmeona matokeo ambayo Yehova* alileta,+ kwamba Yehova* ni mwenye upendo mwororo sana* na mwenye rehema.+

12 Zaidi ya yote, akina ndugu, acheni kuapa kwa mbingu au kwa dunia au kwa kiapo kingine chochote. Bali acheni “Ndiyo” yenu iwe ndiyo, na “Siyo” yenu, siyo,+ ili msihukumiwe.

13 Je, kuna yeyote kati yenu aliye na matatizo? Na aendelee kusali.+ Je, kuna yeyote mwenye roho changamfu? Na aimbe zaburi.+ 14 Je, kuna yeyote aliye mgonjwa kati yenu? Na awaite wazee+ wa kutaniko, nao wasali kwa ajili yake, wakimpaka mafuta+ katika jina la Yehova.* 15 Na sala ya imani itamponya huyo mgonjwa,* na Yehova* atamwinua. Pia, ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.

16 Kwa hiyo ungameni waziwazi dhambi zenu+ kwa mtu na mwenzake na kusali kwa ajili ya mtu na mwenzake, ili mponywe. Dua ya mtu mwadilifu ina nguvu nyingi.*+ 17 Eliya alikuwa mtu mwenye hisia kama zetu, na bado aliposali kwa bidii mvua isinyeshe, haikunyesha juu ya nchi kwa miaka mitatu na miezi sita.+ 18 Naye akasali tena, na mbingu ikatoa mvua na nchi ikazaa matunda.+

19 Ndugu zangu, yeyote kati yenu akipotoshwa kutoka katika kweli na mwingine amrudishe, 20 jueni kwamba yeyote anayemrudisha mtenda dhambi kutoka kwenye kosa+ la njia yake atamwokoa* kutoka kwenye kifo naye atafunika dhambi nyingi.+

Au “bila kutafuta makosa.”

Angalia Nyongeza A5.

Tnn., “ajivunie.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “ kunaswa kama kwa kutumia chambo.”

Au “ambaye habadiliki kama kugeuka kwa kivuli.”

Au labda, “wingi wa ubaya.”

Au “kuokoa nafsi zenu.”

Au “uso wake wa asili.”

Au “ni mtu wa dini.”

Au “hauongozi kwa lijamu.”

Au “dini.”

Au “inawakaripia.”

Tnn., “sheria ya uhuru.”

Tnn., “wako uchi.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “pumzi.”

Au “kali.”

Au “hufanya makosa.”

Tnn., “mzunguko wa uhai (chanzo).”

Angalia Kamusi.

Angalia Nyongeza A5.

Au “yasiyo na chumvi.”

Au “yasiyo na chumvi.”

Au labda, “tamaa ya kupata mambo makuu.”

Au labda, “tamaa ya kupata mambo makuu.”

Au labda, “na.”

Tnn., “ndani ya viungo vyenu.”

Au “ Enyi msio waaminifu.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Aina ya wadudu.

Angalia Nyongeza A5.

Au “Msizomeane; Msilalamikiane.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “wamebarikiwa.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “ni mwenye huruma sana.”

Angalia Nyongeza A5.

Au labda, “aliyechoka.”

Angalia Nyongeza A5.

Tnn., “ina nguvu nyingi inapofanya kazi.”

Au “ataokoa nafsi yake.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki