BARUA YA KWANZA YA PETRO
1 Petro, mtume+ wa Yesu Kristo, kwa wakaaji wa muda waliotawanyika katika Ponto, Galatia, Kapadokia,+ Asia, na Bithinia, kwa wale waliochaguliwa 2 kulingana na ujuzi wa awali wa Mungu aliye Baba,+ kwa kutakaswa kwa roho,+ kusudi wawe watiifu na kunyunyiziwa damu ya Yesu Kristo:+
Na mwongezewe fadhili zisizostahiliwa na amani.
3 Asifiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwa maana kulingana na rehema yake kubwa alituzaa sisi upya+ kwenye tumaini lililo hai+ kupitia ufufuo wa Yesu Kristo kutoka kwa wafu,+ 4 kwenye urithi usioharibika na usio na unajisi na usiofifia.+ Urithi huo umewekwa akiba mbinguni kwa ajili yenu,+ 5 ninyi mnaolindwa kwa nguvu za Mungu kupitia imani kwa ajili ya wokovu ulio tayari kufunuliwa katika kipindi cha mwisho cha wakati. 6 Kwa sababu ya jambo hilo mnashangilia sana, ingawa kwa muda mfupi, ikiwa ni lazima, mmehuzunishwa kwa majaribu mbalimbali,+ 7 ili sifa iliyojaribiwa ya imani yenu,+ iliyo na thamani kubwa zaidi kuliko dhahabu ambayo huharibika ijapokuwa inajaribiwa* kwa moto, ipatikane kuwa sababu ya sifa na utukufu na heshima wakati wa ufunuo wa Yesu Kristo.+ 8 Mnampenda ingawa hamkumwona kamwe. Ijapokuwa hammwoni sasa, bado mnaonyesha imani katika yeye na mnashangilia sana kwa shangwe isiyoelezeka na iliyotukuka, 9 huku mkifikia lengo la* imani yenu, wokovu wenu.*+
10 Kuhusu wokovu huu, manabii waliotoa unabii kuhusu fadhili zisizostahiliwa zilizokusudiwa kwa ajili yenu, walifanya uchunguzi kwa bidii na kutafuta kwa uangalifu.+ 11 Waliendelea kuchunguza wakati hususa au majira ambayo roho iliyokuwa ndani yao ilikuwa ikionyesha kumhusu Kristo+ ilipokuwa ikitoa ushahidi mapema kuhusu mateso ya Kristo+ na kuhusu utukufu ambao ungefuata. 12 Walifunuliwa kwamba hawakuwa wakijihudumia wenyewe, bali walikuwa wakiwahudumia ninyi, kwa mambo ambayo sasa mmetangaziwa na wale ambao waliwatangazia habari njema kwa roho takatifu iliyotumwa kutoka mbinguni.+ Malaika wanatamani kuchungulia ndani ya mambo hayo.
13 Kwa hiyo kazeni akili zenu kwa ajili ya utendaji;+ tunzeni akili zenu kwa ukamili;+ kazeni tumaini lenu juu ya fadhili zisizostahiliwa zitakazoletwa kwenu wakati wa ufunuo wa Yesu Kristo. 14 Kama watoto watiifu, acheni kufinyangwa* na tamaa mlizokuwa nazo zamani katika hali yenu ya kutojua, 15 lakini iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote kama Yule Mtakatifu aliyewaita ninyi,+ 16 kwa maana imeandikwa: “Lazima muwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.”+
17 Na ikiwa mnamwitia Baba ambaye huhukumu bila ubaguzi+ kulingana na matendo ya kila mmoja, jiendesheni kwa kuogopa+ wakati ambao ninyi ni wakaaji wa muda. 18 Kwa maana mnajua kwamba mliwekwa huru*+ kutoka kwenye mwenendo wenu usio na faida ambao mlipokea kutoka kwa mababu zenu,* si kwa vitu vyenye kuharibika, kwa fedha au dhahabu, 19 bali ilikuwa kwa damu yenye thamani,+ kama ile ya mwanakondoo asiye na dosari+ na asiye na doa, ile ya Kristo.+ 20 Ni kweli, yeye alijulikana mapema kabla ya kuwekwa msingi wa ulimwengu,+ lakini alifunuliwa mwishoni mwa nyakati kwa ajili yenu.+ 21 Kupitia yeye mnamwamini Mungu,+ yule aliyemfufua kutoka kwa wafu+ na kumpa utukufu,+ ili imani na tumaini lenu liwe katika Mungu.
22 Sasa kwa sababu mmejitakasa wenyewe* kwa kuwa watiifu kwa ile kweli na hivyo kuwa na upendo wa kindugu+ bila unafiki, pendaneni sana kutoka moyoni.+ 23 Kwa maana mmezaliwa upya,+ si kupitia mbegu* yenye kuharibika, bali kupitia ile isiyoharibika,+ kupitia neno la Mungu aliye hai na anayedumu.+ 24 Kwa maana “wote wenye mwili ni kama nyasi, na utukufu wao wote ni kama ua la shambani; nyasi hukauka, na ua huanguka, 25 bali neno la Yehova* linadumu milele.”+ Na “neno” hilo ni habari njema mliyotangaziwa.+
2 Basi, acheni ubaya wote+ na udanganyifu na unafiki na wivu na masengenyo. 2 Kama watoto wachanga waliozaliwa hivi karibuni,+ kuzeni hamu kwa ajili ya maziwa yasiyochanganywa na kitu* ya lile neno, ili kupitia hayo mkue kufikia wokovu,+ 3 mradi tu mmeonja na kuona kwamba Bwana ni mwenye fadhili.
4 Mkimjia yeye, jiwe lililo hai lililokataliwa na wanadamu+ bali lililochaguliwa na lenye thamani kwa Mungu,+ 5 ninyi wenyewe pia kama mawe yaliyo hai mnajengwa kuwa nyumba ya kiroho+ kusudi muwe ukuhani mtakatifu, ili kutoa dhabihu za kiroho+ zenye kukubalika kwa Mungu kupitia Yesu Kristo.+ 6 Kwa maana Andiko linasema: “Tazama! Ninaweka katika Sayuni jiwe lililochaguliwa, jiwe la pembeni la msingi lenye thamani, na yeyote anayeonyesha imani katika hilo hatakata tamaa kamwe.”*+
7 Kwa hiyo, yeye ni mwenye thamani kwenu, kwa sababu ninyi ni waamini; lakini kwa wale wasioamini, “jiwe ambalo wajenzi walilikataa+ limekuwa jiwe kuu la pembeni”*+ 8 na “jiwe la kukwaza na mwamba wa kuangusha.”+ Wanajikwaa kwa sababu hawatii lile neno. Waliwekwa rasmi pia kwa kusudi hilo. 9 Lakini ninyi ni “jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu,+ na watu walio mali ya pekee,+ ili mtangaze kotekote sifa bora”*+ za Yule aliyewaita kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.+ 10 Kwa kuwa wakati fulani ninyi hamkuwa watu, lakini sasa ninyi ni watu wa Mungu;+ hamkuwa mmeonyeshwa rehema, lakini sasa mmeonyeshwa rehema.+
11 Wapendwa, ninawahimiza ninyi kama wageni na wakaaji wa muda+ kwamba mwendelee kujiepusha na tamaa za mwili,+ ambazo hupigana vita nanyi.*+ 12 Dumisheni mwenendo wenu ukiwa mzuri kati ya mataifa,+ ili wanapowashutumu kuwa watenda dhambi, washuhudie kwa macho yao matendo yenu mazuri+ na hivyo wamtukuze Mungu katika siku ya ukaguzi wake.
13 Kwa ajili ya Bwana jitiisheni wenyewe kwa kila kitu kilichofanywa na binadamu,*+ iwe ni kwa mfalme+ akiwa mkubwa 14 au kwa magavana wakiwa kama wametumwa naye kuwaadhibu watenda maovu lakini kuwasifu wanaotenda mema.+ 15 Kwa maana ni mapenzi ya Mungu kwamba kwa kutenda mema mnyamazishe* maneno ya kijinga ya watu wasio na akili.+ 16 Iweni kama watu huru,+ mkitumia uhuru wenu, si kama kifuniko* cha kufanya mabaya,+ bali kama watumwa wa Mungu.+ 17 Waheshimuni watu wa namna zote,+ upendeni ushirika mzima wa akina ndugu,*+ mwogopeni Mungu,+ mheshimuni mfalme.+
18 Watumishi na wajitiishe kwa mabwana wao kwa woga unaofaa,+ si kwa wale tu walio wema na wapole, bali pia kwa wale ambao ni wagumu kupendeza. 19 Kwa maana inakubalika ikiwa mtu anavumilia taabu* na kuteseka isivyo haki kwa sababu ya dhamiri kwa Mungu.+ 20 Kwa maana kuna faida gani ikiwa mnavumilia mnapopigwa kwa kufanya dhambi?+ Lakini ikiwa mnavumilia mateso kwa sababu ya kufanya mema, jambo hilo linakubalika kwa Mungu.+
21 Kwa kweli, mliitwa kwenye mwendo huu, kwa sababu hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu,+ akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.+ 22 Yeye hakufanya dhambi,+ wala udanganyifu haukupatikana kinywani mwake.+ 23 Alipokuwa akitukanwa,*+ hakujibu kwa kutukana.*+ Alipokuwa akiteseka,+ hakutoa vitisho, bali alijikabidhi mkononi mwa Yule anayehukumu+ kwa uadilifu. 24 Yeye mwenyewe alichukua dhambi zetu+ katika mwili wake mwenyewe juu ya mti,+ ili tufe kuhusiana* na dhambi na tuishi kuhusiana na uadilifu. Na “kwa vidonda vyake mliponywa.”+ 25 Kwa maana mlikuwa kama kondoo wanaopotea njia,+ lakini sasa mmerudi kwa mchungaji+ na mwangalizi wa nafsi zenu.*
3 Vivyo hivyo, ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu,+ ili ikiwa kuna wale wasiotii lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao,+ 2 kwa sababu wameshuhudia kwa macho yao mwenendo wenu ulio safi kiadili+ pamoja na heshima kubwa. 3 Kujipamba kwenu kusiwe kwa nje—kusuka nywele na kuvaa mapambo ya dhahabu+ au mavazi bora— 4 bali kuwe yule mtu wa siri wa moyoni katika mapambo yasiyoharibika ya roho ya utulivu na ya upole,+ ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu. 5 Kwa maana hapo zamani ndivyo walivyokuwa wakijipamba wale wanawake watakatifu, waliomtumaini Mungu, wakijitiisha kwa waume zao, 6 kama Sara alivyomtii Abrahamu, akimwita bwana.+ Nanyi mmekuwa watoto wake, mradi tu mnaendelea kutenda mema, bila kuogopa.+
7 Enyi waume, vivyo hivyo endeleeni kukaa nao kulingana na ujuzi.* Wapeni heshima+ kama chombo dhaifu zaidi, yaani, mwanamke, kwa kuwa wao pia ni warithi pamoja nanyi+ wa pendeleo lisilostahiliwa la uzima, ili sala zenu zisizuiwe.
8 Mwishowe, ninyi nyote fikirini kwa upatano,*+ muwe na hisia-mwenzi, upendo wa kindugu, huruma nyororo,+ na unyenyekevu.+ 9 Msilipe ubaya kwa ubaya+ au matukano kwa matukano.+ Badala yake, lipeni kwa baraka,+ kwa sababu mliitwa kwenye mwendo huu, ili mrithi baraka.
10 Kwa maana “yeyote anayependa uzima na kuona siku zilizo njema, lazima aulinde ulimi wake usiseme mabaya+ na midomo yake isiseme udanganyifu. 11 Na aache mabaya,+ atende mema;+ na atafute amani na kuifuatilia.+ 12 Kwa maana macho ya Yehova* yanawatazama waadilifu, na masikio yake yanasikiliza dua yao,+ lakini uso wa Yehova* uko dhidi ya wale wanaotenda maovu.”+
13 Kwa kweli, ni nani atakayewadhuru mkifanya yaliyo mema kwa bidii?+ 14 Lakini hata mkiteseka kwa ajili ya uadilifu, ninyi ni wenye furaha.+ Hata hivyo, msiogope kile wanachokiogopa,* wala msiwe na wasiwasi.+ 15 Bali mtakaseni Kristo kuwa Bwana katika mioyo yenu, sikuzote mkiwa tayari kujitetea mbele ya kila mtu anayewauliza sababu ya tumaini mlilo nalo, lakini mkifanya hivyo kwa upole+ na heshima kubwa.+
16 Iweni na dhamiri njema,+ ili katika kila jambo ambalo wanasema vibaya dhidi yenu, wale wanaosema vibaya dhidi yenu waaibishwe+ kwa sababu ya mwenendo wenu mzuri mkiwa wafuasi wa Kristo.+ 17 Kwa maana ni afadhali kuteseka kwa sababu mnatenda mema,+ ikiwa ni mapenzi ya Mungu kuruhusu jambo hilo, kuliko kuteseka kwa sababu mnatenda maovu.+ 18 Kwa maana Kristo alikufa mara moja kwa wakati wote kwa ajili ya dhambi,+ mtu mwadilifu kwa ajili ya wasio waadilifu,+ ili awaongoze ninyi kwa Mungu.+ Aliuawa katika mwili,+ lakini akafanywa kuwa hai katika roho.+ 19 Na katika hali hiyo alienda na kuwahubiria roho walio gerezani,+ 20 ambao mwanzoni hawakuwa watiifu Mungu alipokuwa akingoja kwa subira* katika siku za Noa,+ safina ilipokuwa ikijengwa,+ ambayo ndani yake watu wachache, yaani, nafsi nane,* walichukuliwa salama kupitia maji.+
21 Ubatizo, ambao unalingana na hili, unawaokoa ninyi sasa pia (si kwa kuondoa uchafu wa mwili, bali kwa ombi linalotolewa kwa Mungu ili kupata dhamiri njema),+ kupitia ufufuo wa Yesu Kristo. 22 Yeye yuko kwenye mkono wa kuume wa Mungu,+ kwa maana alienda mbinguni, nao malaika na mamlaka na nguvu vilitiishwa kwake.+
4 Kwa kuwa Kristo aliteseka katika mwili,+ ninyi pia jiimarisheni kwa mwelekeo uleule wa akili;* kwa sababu mtu ambaye ameteseka katika mwili ameachana na dhambi,+ 2 ili aishi wakati wake uliobaki katika mwili, si kwa ajili ya tamaa za wanadamu tena,+ bali kwa ajili ya mapenzi ya Mungu.+ 3 Kwa maana wakati uliopita uliwatosha kufanya mapenzi ya mataifa,+ mlipofanya vitendo vya mwenendo mpotovu,* uchu, kunywa kupita kiasi, karamu zenye vurugu,* mashindano ya kunywa, na ibada za sanamu zenye kuchukiza.+ 4 Wanashangaa kwa sababu hamwendelei kukimbia pamoja nao katika mwendo uliooza wa upotovu, basi wanawatukana ninyi.+ 5 Lakini watu hao watatoa hesabu kwa yule aliye tayari kuhukumu walio hai na waliokufa.+ 6 Kwa kweli, hiyo ndiyo sababu habari njema ilitangazwa kwa wafu pia,+ ili ingawa wanahukumiwa katika mwili kwa maoni ya wanadamu, waishi kwa kupatana na roho kwa maoni ya Mungu.
7 Lakini mwisho wa mambo yote umekaribia. Kwa hiyo, iweni na utimamu wa akili,+ na kukesha* kuhusiana na sala.+ 8 Zaidi ya mambo yote, pendaneni sana,+ kwa sababu upendo hufunika dhambi nyingi.+ 9 Mkaribishane bila kunung’unika.+ 10 Kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni kuhudumiana kama wasimamizi wazuri wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu zinazoonyeshwa kwa njia mbalimbali.+ 11 Yeyote akisema, na afanye hivyo kana kwamba anasema maneno matakatifu kutoka kwa Mungu; yeyote akihudumu, na afanye hivyo kama anayetegemea nguvu ambazo Mungu hutoa;+ ili katika mambo yote Mungu atukuzwe+ kupitia Yesu Kristo. Utukufu na nguvu ni zake milele na milele. Amina.
12 Wapendwa, msishangazwe na majaribu makali* yanayowapata,+ kana kwamba mnapatwa na jambo geni. 13 Badala yake, endeleeni kushangilia+ kwa kadiri ambayo ninyi ni washiriki katika mateso ya Kristo,+ ili mshangilie na kuwa na shangwe sana pia wakati wa ufunuo wa utukufu wake.+ 14 Ikiwa mnashutumiwa* kwa ajili ya jina la Kristo, ninyi ni wenye furaha,+ kwa sababu roho ya utukufu, yaani roho ya Mungu, inatulia juu yenu.
15 Hata hivyo, yeyote kati yenu asiteseke kwa sababu yeye ni muuaji au mwizi au mkosaji au mtu anayejiingiza katika mambo ya watu wengine.+ 16 Lakini yeyote akiteseka kwa sababu ni Mkristo, asione aibu,+ bali na aendelee kumtukuza Mungu huku akilibeba jina hili. 17 Kwa maana ni wakati uliowekwa wa hukumu kuanza na nyumba ya Mungu.+ Sasa ikiwa inaanza na sisi kwanza,+ basi matokeo kwa wale wasiotii habari njema ya Mungu yatakuwaje?+ 18 “Na ikiwa mtu mwadilifu anaokolewa kwa shida, itakuwaje kwa mtu asiyemwogopa Mungu na mtenda dhambi?”+ 19 Hivyo basi, acheni wale wanaoteseka kwa kufanya mapenzi ya Mungu waendelee kujikabidhi wenyewe* kwa Muumba mwaminifu wanapotenda mema.+
5 Kwa hiyo, nikiwa mzee pia, shahidi wa mateso ya Kristo, na mshiriki wa utukufu utakaofunuliwa,+ ninawasihi* wazee miongoni mwenu: 2 Lichungeni kundi la Mungu+ lililo chini ya utunzaji wenu, mkiwa waangalizi,* si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari mbele za Mungu;+ si kwa kupenda pato lisilo la haki,+ bali kwa hamu; 3 si kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu,+ bali kuwa vielelezo kwa kundi.+ 4 Na mchungaji mkuu+ atakapofunuliwa, mtapokea taji la utukufu lisilofifia.+
5 Vivyo hivyo, enyi vijana, jitiisheni kwa wanaume wazee.*+ Lakini ninyi nyote mtendeane kwa* unyenyekevu,* kwa sababu Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.+
6 Kwa hiyo, jinyenyekezeni chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu, ili awainue kwa wakati unaofaa,+ 7 huku mkitupa mahangaiko* yenu yote juu yake,+ kwa sababu yeye anawajali ninyi.+ 8 Tunzeni akili zenu, iweni waangalifu!+ Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.*+ 9 Lakini chukueni msimamo dhidi yake,+ mkiwa imara katika imani, mkijua kwamba mateso yaleyale yanaupata ushirika mzima wa ndugu zenu* ulimwenguni.+ 10 Lakini, baada ya kuteseka kwa muda mfupi, Mungu wa fadhili zote zisizostahiliwa, aliyewaita kwenye utukufu wake wa milele+ katika muungano na Kristo, yeye mwenyewe atamaliza mazoezi yenu. Atawafanya muwe imara,+ atawatia nguvu,+ atawapa msingi imara. 11 Na awe na nguvu milele. Amina.
12 Kupitia Silvano,*+ ambaye ninamwona kuwa ndugu mwaminifu, nimewaandikia kwa maneno machache, ili kuwatia moyo na kutoa ushahidi kwa bidii kwamba hizi ndizo fadhili zisizostahiliwa za Mungu. Simameni imara katika fadhili hizo. 13 Mwanamke aliye Babiloni, aliyechaguliwa kama ninyi, anawatumia salamu zake, na vilevile Marko,+ mwanangu. 14 Salimianeni kwa busu la upendo.
Na muwe na amani ninyi nyote mlio katika muungano na Kristo.
Au “inasafishwa.”
Au “mradi wa.”
Au “wokovu wa nafsi zenu.”
Au “kufanyizwa kulingana.”
Tnn., “mlilipiwa fidia; mlikombolewa.”
Au “kutokana na desturi.”
Au “mmezitakasa nafsi zenu.”
Yaani, mbegu inayoweza kuzaa, au inayotokeza matunda.
Angalia Nyongeza A5.
Au “maziwa safi; maziwa halisi.”
Tnn., “hataaibika.”
Tnn., “kichwa cha pembeni.”
Yaani, sifa zake nzuri na matendo mazuri.
Au “na nafsi zenu.”
Au “shirika la kibinadamu.”
Tnn., “mzibe.”
Au “kisingizio.”
Tnn., “undugu.”
Au “ huzuni; maumivu.”
Au “akishutumiwa.”
Au “hakushutumu.”
Au “tuachane.”
Au “wa uhai wenu.”
Au “mkiwafikiria na kuwajali; kuwaelewa.”
Au “kwa umoja wa akili.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Au labda, “msiogope vitisho vyao.”
Tnn., “subira ya Mungu ilikuwa ikingoja.”
Au “watu wanane.”
Au “azimio lilelile; uamuzi uleule.”
Au “ufidhuli; matendo ya kuchukiza yanayofanywa bila aibu.” Kigiriki, a·selʹgei·a. Angalia Kamusi.
Au “karamu za kupindukia.”
Au “muwe chonjo; muwe macho.”
Au “majaribu kama moto.”
Au “mnatukanwa.”
Au “kuzikabidhi nafsi zao.”
Au “ninawahimiza.”
Au “mkililinda kwa makini.”
Au “wazee.”
Au “mjifunge; mjivike.”
Au “unyenyekevu wa akili.”
Au “matatizo; wasiwasi wenu wote.”
Au “akimtafuta mtu ili ammeze.”
Tnn., “undugu wenu.”
Pia anaitwa Sila.