Danieli
5 Mfalme Belshaza+ naye alifanya karamu kwa ajili ya wakuu wake elfu, naye akanywa divai mbele ya hao elfu.+ 2 Akiwa amechochewa na divai,+ Belshaza akasema viletwe vyombo vya dhahabu na fedha+ ambavyo Nebukadneza baba yake alikuwa amevichukua kutoka hekalu lililokuwa Yerusalemu, ili mfalme na wakuu wake, masuria wake na wake zake wadogo wavinywee.+ 3 Basi wakavileta ndani vile vyombo vya dhahabu ambavyo walikuwa wamevitoa katika hekalu la Mungu lililokuwa Yerusalemu, naye mfalme na wakuu wake, masuria wake na wake zake wadogo wakavinywea. 4 Wakanywa divai, wakaisifu miungu ya dhahabu na fedha, shaba, chuma, miti na mawe.+
5 Ndipo wakati huohuo vidole vya mkono wa mtu vikatokea na kuandika mbele ya kinara cha taa juu ya lipu ya ukuta wa jumba la mfalme,+ naye mfalme akawa anaona sehemu ya nyuma ya mkono uliokuwa ukiandika. 6 Na wakati huo, kwa habari ya mfalme, sura yake ikabadilika, mawazo yake yakaanza kumwogopesha,+ viungo vya viuno vyake vikalegea,+ magoti yake yakawa yanagongana.+
7 Mfalme akaita kwa sauti kubwa akasema waletwe ndani wafanya-mazingaombwe, Wakaldayo na wanajimu.+ Mfalme akawaambia watu wenye hekima wa Babiloni: “Mtu yeyote atakayesoma maandishi haya na kunionyesha tafsiri yake kamili, atavikwa mavazi ya zambarau,+ pamoja na mkufu wa dhahabu shingoni mwake, naye atakuwa mtawala wa tatu katika ufalme.”+
8 Basi wakaingia watu wote wenye hekima wa mfalme, lakini hawakuwa na uwezo wa kutosha kuweza kusoma maandishi hayo wala kumwambia mfalme tafsiri yake.+ 9 Kwa hiyo Mfalme Belshaza akaogopa sana na rangi ya uso wake ikaanza kubadilika ndani yake; na wakuu wake wakahangaika.+
10 Malkia naye, kwa sababu ya maneno ya mfalme na wakuu wake, akaingia ndani ya jumba la karamu. Malkia akasema: “Ee mfalme, uishi mpaka wakati usio na kipimo.+ Usiache mawazo yako yakuogopeshe, wala rangi ya uso wako ibadilike. 11 Kuna mtu mwenye uwezo katika ufalme wako ambaye ndani yake mna roho ya miungu mitakatifu;+ na katika siku za baba yako nuru na ufahamu na hekima kama hekima ya miungu zilipatikana ndani yake, na baba yako mwenyewe, Mfalme Nebukadneza, akamweka awe mkuu+ wa makuhani wenye kufanya uchawi, na wafanya-mazingaombwe, na Wakaldayo na wanajimu, Ee mfalme; 12 kwa kuwa roho isiyo ya kawaida na ujuzi na ufahamu wa kutafsiri ndoto+ na kueleza vitendawili na kufungua mafundo ilikuwa imepatikana ndani yake,+ ndani ya Danieli, ambaye mfalme alimpa jina Belteshaza.+ Basi Danieli na aitwe, apate kuonyesha tafsiri kamili.”
13 Basi Danieli akaletwa mbele ya mfalme. Mfalme akasema na kumuuliza Danieli: “Je, wewe ndiye Danieli ambaye ni mmoja wa wahamishwa wa Yuda,+ ambao baba yangu mfalme aliwatoa Yuda?+ 14 Nimesikia pia kuhusu wewe kwamba roho ya miungu imo ndani yako,+ na nuru na ufahamu na hekima+ isiyo ya kawaida zimepatikana ndani yako. 15 Basi watu wenye hekima na wafanya-mazingaombwe wameletwa mbele yangu, ili wasome maandishi haya, waniambie tafsiri yake; lakini hawana uwezo wa kutosha kunionyesha tafsiri kamili ya neno hilo.+ 16 Nami mwenyewe nimesikia habari zako, kwamba unaweza kutoa tafsiri+ na kufungua mafundo. Basi, ukiweza kusoma maandishi haya na kunijulisha tafsiri yake kamili, utavikwa mavazi ya zambarau, pamoja na mkufu wa dhahabu shingoni mwako, nawe utakuwa mtawala wa tatu katika ufalme.”+
17 Ndipo Danieli akajibu na kusema mbele ya mfalme: “Zawadi zako na ziwe zako mwenyewe, na tuzo zako uwape wengine.+ Hata hivyo, mimi nitamsomea mfalme maandishi haya, nami nitamjulisha tafsiri yake.+ 18 Basi wewe, Ee mfalme, Mungu Aliye Juu Zaidi+ alimpa baba yako Nebukadneza+ ufalme na ukuu na heshima na utukufu wa enzi.+ 19 Na kwa sababu ya ukuu ambao Yeye alimpa, vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vilitetemeka na kuogopa mbele yake.+ Mtu yeyote aliyetaka kumuua, alimuua; mtu yeyote aliyetaka kumpiga, alimpiga; na mtu yeyote aliyetaka kumwinua, alimwinua; na mtu yeyote aliyetaka kumfedhehesha, alimfedhehesha.+ 20 Lakini moyo wake ulipojivuna na roho yake ikawa ngumu, akatenda kwa kimbelembele,+ alishushwa kutoka katika kiti cha ufalme wake, akaondolewa heshima yake.+ 21 Naye akafukuziwa mbali kutoka kati ya wanadamu, na moyo wake ukafanywa kama ule wa mnyama, naye akakaa pamoja na punda-mwitu.+ Wakawa wanampa majani ale kama ng’ombe, mwili wake ukalowa maji kwa umande wa mbingu,+ mpaka alipojua kwamba Mungu Aliye Juu Zaidi ni Mtawala katika ufalme wa wanadamu, na kwamba humweka juu yake yeyote yule anayemtaka.+
22 “Na wewe, Belshaza mwana wake,+ hukunyenyekeza moyo wako,+ ijapokuwa ulijua hayo yote.+ 23 Bali ulijiinua juu ya Bwana wa mbingu,+ nao wakaleta mbele yako vyombo vya nyumba yake;+ na wewe pamoja na wakuu wako, masuria wako na wake zako wadogo mmekuwa mkivinywea divai. Nawe umeisifu miungu minyonge ya fedha na ya dhahabu, shaba, chuma, miti na mawe,+ ambayo haioni chochote, wala kusikia chochote, wala kujua chochote;+ lakini hukumtukuza+ Mungu ambaye pumzi yako imo mkononi mwake+ na ambaye njia zako zote ni zake.+ 24 Basi sehemu ya nyuma ya mkono ilitumwa kutoka mbele zake, na maandishi haya yakaandikwa.+ 25 Na haya ndiyo maandishi ambayo yaliandikwa: MENE, MENE, TEKELI na PARSINI.
26 “Hii ndiyo tafsiri ya neno: MENE, Mungu amehesabu siku za ufalme wako naye ameukomesha.+
27 “TEKELI, wewe umepimwa katika mizani, ukaonekana kuwa umepungukiwa.+
28 “PERESI, ufalme wako umegawanywa na kupewa Wamedi na Waajemi.”+
29 Ndipo Belshaza akatoa amri, nao wakamvika Danieli mavazi ya zambarau, pamoja na mkufu wa dhahabu shingoni mwake; nao wakatangaza kumhusu yeye kwamba atakuwa mtawala wa tatu katika ufalme.+
30 Usiku huohuo Belshaza mfalme Mkaldayo akauawa,+ 31 naye Dario+ Mmedi akaupokea ufalme, akiwa na umri wa kama miaka 62.