KWA WAEFESO
1 Paulo, mtume wa Kristo Yesu kupitia mapenzi ya Mungu, kwa watakatifu walio huko Efeso+ na walio waaminifu katika muungano na Kristo Yesu:
2 Na muwe na fadhili zisizostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo.
3 Asifiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwa kuwa ametubariki kwa kila baraka ya kiroho katika mahali pa kimbingu katika muungano na Kristo,+ 4 kama alivyotuchagua tuwe katika muungano naye* kabla ya kuwekwa msingi wa ulimwengu, ili tuwe watakatifu na bila dosari+ mbele zake katika upendo. 5 Kwa maana alituagiza awali+ tufanywe kuwa wanawe mwenyewe+ kupitia Yesu Kristo, kulingana na mapenzi yake mema na kusudi lake,+ 6 kwa sifa ya fadhili zake zisizostahiliwa+ zenye utukufu alizotupatia kwa fadhili kupitia mpendwa wake.+ 7 Kupitia kwake tunaachiliwa huru kwa njia ya fidia kupitia damu ya huyo,+ ndiyo, msamaha wa makosa yetu,+ kulingana na utajiri wa fadhili zake zisizostahiliwa.
8 Alituzidishia fadhili zisizostahiliwa katika hekima yote na uelewaji,* 9 kwa kutujulisha siri takatifu+ ya mapenzi yake. Ni kulingana na mapenzi yake mema aliyokusudia mwenyewe 10 kwa ajili ya usimamizi* kwenye nyakati kamili zilizowekwa, kukusanya pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.+ Ndiyo, katika yeye 11 ambaye tuko katika muungano naye na tulihesabiwa kuwa warithi,+ kwa kuwa tuliagizwa awali kulingana na kusudi la yule anayetimiza mambo yote kama anavyoamua kulingana na mapenzi yake, 12 ili sisi tulio wa kwanza kumtumaini Kristo tutumikie kwa ajili ya sifa ya utukufu wake. 13 Lakini ninyi pia mlimtumaini baada ya kulisikia neno la kweli, habari njema kuhusu wokovu wenu. Baada ya kuamini, mlitiwa muhuri+ kupitia kwake kwa roho takatifu iliyoahidiwa, 14 ambayo ni rehani ya mapema* ya urithi wetu,+ kwa kusudi la kuachilia huru mali ya Mungu mwenyewe+ kupitia fidia,+ kwa sifa yake yenye utukufu.
15 Hiyo ndiyo sababu mimi pia, kwa kuwa nimesikia kuhusu imani mliyo nayo katika Bwana Yesu na upendo mnaowaonyesha watakatifu wote, 16 siachi kamwe kutoa shukrani kwa ajili yenu. Ninaendelea kuwataja katika sala zangu, 17 ili Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa utukufu, awape roho ya hekima na ya ufunuo katika ujuzi sahihi kumhusu.+ 18 Ameyatia nuru macho ya moyo wenu, ili mjue tumaini alilowaitia, utajiri wenye utukufu ambao amewawekea watakatifu kuwa urithi,+ 19 na jinsi nguvu zake kutuelekea sisi waamini zilivyo kuu zaidi.+ Ni kulingana na utendaji wa uwezo wa nguvu zake, 20 ambao aliutumia kuhusiana na Kristo alipomfufua kutoka kwa wafu na kumketisha kwenye mkono wake wa kuume+ katika mahali pa kimbingu, 21 juu kuliko kila serikali na mamlaka na nguvu na utawala na kila jina linalotajwa,+ si katika mfumo huu wa mambo* tu, bali pia katika ule unaokuja. 22 Alivitiisha pia vitu vyote chini ya miguu yake+ na kumfanya kuwa kichwa juu ya vitu vyote kuhusiana na kutaniko,+ 23 ambalo ni mwili wake,+ ujazo wake anayejaza vitu vyote katika vyote.
2 Zaidi ya hayo, Mungu aliwafanya muwe hai, ingawa mlikuwa wafu katika makosa na dhambi zenu,+ 2 ambazo wakati fulani mlitembea ndani yake kulingana na mfumo wa mambo* wa ulimwengu huu,+ kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewa,+ roho+ ambayo sasa inafanya kazi katika wana wa kutotii. 3 Ndiyo, wakati fulani sisi sote tulijiendesha miongoni mwao kupatana na tamaa za mwili wetu,+ tukifanya mapenzi ya mwili na ya fikira zetu,+ nasi kiasili tulikuwa watoto wa ghadhabu+ kama wale wengine. 4 Lakini Mungu, akiwa tajiri katika rehema,+ kwa sababu ya upendo wake mwingi aliotupenda nao,+ 5 alitufanya hai pamoja na Kristo, hata tulipokuwa wafu katika makosa+—mmeokolewa kupitia fadhili zisizostahiliwa. 6 Isitoshe, alituinua pamoja na kutuketisha pamoja mahali pa kimbingu katika muungano na Kristo Yesu,+ 7 ili kwenye mifumo ya mambo* inayokuja aonyeshe utajiri mwingi zaidi wa fadhili zake zisizostahiliwa katika neema yake* kutuelekea katika muungano na Kristo Yesu.
8 Kwa fadhili hizi zisizostahiliwa, ninyi mmeokolewa kupitia imani,+ na si ninyi mliofanya hivyo; badala yake, ni zawadi ya Mungu. 9 Hapana, si kutokana na matendo,+ ili mtu yeyote asiwe na sababu za kujisifu. 10 Sisi ni kazi ya mikono* ya Mungu na tuliumbwa+ katika muungano na Kristo Yesu+ kwa ajili ya matendo mema, ambayo Mungu aliamua awali ili tutembee katika hayo.
11 Kwa hiyo, kumbukeni kwamba wakati fulani ninyi, watu wa mataifa kwa kuzaliwa, mlikuwa mkiitwa “watu wasiotahiriwa” na wale walioitwa “watu waliotahiriwa,” kutahiriwa ambako kumefanywa mwilini kwa mikono ya wanadamu. 12 Wakati huo hamkuwa na Kristo, mlikuwa mmetengwa na taifa la Israeli, mlikuwa wageni kwa maagano ya ahadi;+ hamkuwa na tumaini na mlikuwa bila Mungu katika ulimwengu.+ 13 Lakini sasa katika muungano na Kristo Yesu ninyi ambao wakati fulani mlikuwa mbali sana, mmekuwa karibu kupitia damu ya Kristo. 14 Kwa maana yeye ni amani yetu,+ yule aliyefanya vile vikundi viwili kuwa kimoja+ na kuuharibu ukuta wa katikati uliowatenganisha.+ 15 Kupitia mwili wake aliufuta uadui, ile Sheria iliyokuwa na amri na maagizo, ili afanye vile vikundi viwili katika muungano na yeye mwenyewe viwe mtu mmoja mpya+ na kufanya amani, 16 na kuvipatanisha kikamili vile vikundi viwili vya watu katika mwili mmoja kwa Mungu kupitia mti wa mateso,*+ kwa sababu alikuwa ameua ule uadui+ kupitia yeye mwenyewe. 17 Naye alikuja na kuwatangazia habari njema ya amani ninyi mliokuwa mbali sana, na amani kwa wale waliokuwa karibu, 18 kwa sababu kupitia kwake, sisi, vikundi viwili vya watu, tuna uhuru wa kumkaribia Baba kwa roho moja.
19 Basi ninyi si wageni tena na watu wa mataifa ya kigeni,+ bali ninyi ni raia wenzi+ wa watakatifu na ni washiriki wa nyumba ya Mungu,+ 20 nanyi mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii,+ naye Kristo Yesu mwenyewe ndiye jiwe la msingi la pembeni.+ 21 Katika muungano naye, jengo lote likiwa limeunganishwa kwa upatano,+ linakua ili kuwa hekalu takatifu kwa ajili ya Yehova.*+ 22 Katika muungano naye, ninyi pia mnajengwa pamoja muwe mahali pa Mungu pa kukaa kupitia roho.+
3 Kwa sababu hii, mimi Paulo, mfungwa+ wa Kristo Yesu kwa ajili yenu, watu wa mataifa— 2 ikiwa, kwa kweli, mmesikia kuhusu usimamizi+ wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu ambao nilipewa kwa ajili yenu, 3 kwamba nilijulishwa siri takatifu kupitia ufunuo, kama vile nilivyoandika kwa ufupi hapo mwanzoni. 4 Basi mnaposoma jambo hili, mnaweza kuona jinsi ninavyoelewa siri takatifu+ ya Kristo. 5 Katika vizazi vingine wanadamu hawakujulishwa siri hii kama vile ambavyo sasa imefunuliwa kwa mitume wake watakatifu na manabii kupitia roho,+ 6 yaani, kwamba watu wa mataifa, katika muungano na Kristo Yesu na kupitia habari njema, wawe warithi na viungo vya mwili uleule+ na washiriki wa ahadi pamoja nasi. 7 Mimi nilikuja kuwa mhudumu wa hilo kulingana na zawadi ya bure ya Mungu ya fadhili zisizostahiliwa nilizopewa kupitia utendaji wa nguvu zake.+
8 Mimi, niliye mdogo kuliko aliye mdogo zaidi kati ya watakatifu wote,+ nilipewa fadhili hizi zisizostahiliwa,+ ili niwatangazie mataifa habari njema kuhusu utajiri usiopimika wa Kristo 9 na kufanya kila mtu aone usimamizi wa siri takatifu+ ambayo imefichwa kwa vizazi na vizazi katika Mungu, aliyeumba vitu vyote. 10 Ilikuwa hivyo ili sasa, kupitia kutaniko,+ serikali na mamlaka zilizo mahali pa kimbingu zijulishwe hekima ya Mungu inayoonekana kwa njia nyingi sana.+ 11 Hii ni kulingana na kusudi la milele alilofanyiza kuhusiana na Kristo,+ Yesu Bwana wetu, 12 ambaye kupitia kwake tuna uhuru huu wa kusema na uhuru wa kukaribia+ tukiwa na uhakika kupitia imani yetu kwake. 13 Basi ninawaomba msife moyo kwa sababu ya dhiki zangu kwa ajili yenu, kwa maana zinamaanisha utukufu kwenu.+
14 Kwa sababu hiyo ninampigia Baba magoti, 15 ambaye kila familia mbinguni na duniani hupata jina kutoka kwake. 16 Ninasali kwamba awawezeshe kulingana na wingi wa utukufu wake ili mfanywe kuwa na uwezo katika mtu mliye kwa ndani,+ mkiwa na nguvu kupitia roho yake, 17 na kupitia imani yenu muwe na Kristo akikaa katika mioyo yenu kwa upendo.+ Iweni na mizizi+ na kuimarishwa juu ya ule msingi,+ 18 ili pamoja na watakatifu wote mweze kufahamu kikamili upana na urefu na kimo na kina, 19 na kuujua upendo wa Kristo,+ unaozidi ujuzi, ili mjawe na ujazo wote ambao Mungu hutoa.
20 Basi kwa yule anayeweza, kulingana na nguvu zake zinazotenda ndani yetu,+ kufanya kwa wingi zaidi kupita mambo yote tunayoomba au tunayofikiri,+ 21 na awe na utukufu kupitia kutaniko na kupitia Kristo Yesu kwa vizazi vyote milele na milele. Amina.
4 Kwa hiyo, mimi mfungwa+ katika Bwana, ninawasihi mtembee kwa kustahili+ mwito mliopokea, 2 kwa unyenyekevu*+ wote na upole, kwa subira,+ mkivumiliana kwa upendo,+ 3 mkijitahidi sana kudumisha roho ya umoja katika kifungo cha muungano cha amani.+ 4 Kuna mwili mmoja,+ na roho moja,+ kama mlivyoitwa kwenye tumaini moja;+ 5 Bwana mmoja,+ imani moja, ubatizo mmoja; 6 Mungu mmoja ambaye ni Baba wa wote, aliye juu ya wote, na kupitia wote na katika wote.
7 Basi kila mmoja wetu alionyeshwa fadhili zisizostahiliwa kulingana na jinsi Kristo alivyopima zawadi hiyo ya bure.+ 8 Kwa maana inasema: “Alipopanda juu alichukua mateka; alitoa wanaume kuwa zawadi.”+ 9 Basi neno “alipopanda,” linamaanisha nini? Linamaanisha kwamba pia alishuka chini, yaani, duniani. 10 Yule aliyeshuka ndiye pia aliyepanda+ juu zaidi ya mbingu zote,+ ili atimize mambo yote.
11 Naye alitoa wengine wawe mitume,+ wengine manabii,+ wengine waeneza injili,*+ wengine wachungaji na walimu,+ 12 ili kuwarekebisha* watakatifu, kwa ajili ya kutimiza huduma, na kuujenga mwili wa Kristo,+ 13 mpaka sote tuwe na umoja* katika imani na tuwe na ujuzi sahihi kumhusu Mwana wa Mungu, na kuwa mtu aliyekomaa kabisa,+ na kufikia kiwango cha kimo kamili cha Kristo. 14 Basi tusiwe tena watoto, tukirushwa huku na huku kama kwa mawimbi na kupeperushwa na kila upepo wa fundisho+ kwa udanganyifu wa watu, kupitia ujanja na njia za hila. 15 Lakini tukisema ukweli, kupitia upendo na tuendelee kukua katika mambo yote ndani ya Kristo, ambaye ni kichwa.+ 16 Kupitia kwake mwili wote+ unaunganishwa na kushirikiana kila kiungo kinapofanya kazi yake. Na kila kiungo kinapofanya kazi vizuri, hilo linafanya mwili ukue na kujijenga katika upendo.+
17 Basi ninasema na kushuhudia katika Bwana, kwamba msiishi tena kama watu wa mataifa wanavyoishi,+ katika ubatili wa akili zao.+ 18 Wako gizani kiakili na wametenganishwa na uzima ambao ni wa Mungu, kwa sababu ya ujinga ulio ndani yao na kwa sababu ya ugumu wa* mioyo yao. 19 Kwa kuwa wamepotoka kabisa kimaadili, wamejiingiza katika mwenendo mpotovu*+ na kufanya mambo machafu ya kila namna kwa pupa.
20 Lakini ninyi hamkujifunza kwamba Kristo yuko hivyo, 21 ikiwa kwa kweli mlimsikia na kufundishwa kupitia kwake, kama vile kweli ilivyo katika Yesu. 22 Mlifundishwa kuvua utu wa zamani+ unaopatana na mwenendo wenu wa zamani na ambao unaharibiwa na tamaa zake za udanganyifu.+ 23 Na mnapaswa kuendelea kufanywa upya katika nguvu zinazoongoza akili zenu,*+ 24 na mnapaswa kuvaa utu mpya+ ulioumbwa kupatana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.
25 Kwa hiyo, kwa sababu mmeacha udanganyifu, semeni ukweli kila mmoja na mwenzake,+ kwa sababu sisi ni viungo vya mwili mmoja.+ 26 Iweni na hasira, lakini msitende dhambi;+ jua lisitue mkiwa bado mmekasirika;+ 27 msimpe Ibilisi nafasi.+ 28 Mwizi asiibe tena; badala yake afanye kazi kwa bidii, akifanya kazi njema kwa mikono yake,+ ili awe na kitu cha kumgawia mtu mwenye uhitaji.+ 29 Neno lililooza lisitoke kinywani mwenu,+ bali neno jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwanufaishe wale wanaolisikia.+ 30 Pia, msiwe mkiihuzunisha roho takatifu ya Mungu,+ ambayo kupitia hiyo mmetiwa muhuri+ kwa ajili ya siku ambayo mtawekwa huru kupitia fidia.+
31 Acheni kabisa kila aina ya chuki yenye uhasama,+ hasira, ghadhabu, kufoka, matusi,+ na mambo yote yanayodhuru.+ 32 Bali mtendeane kwa fadhili, huruma nyororo,+ mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu alivyowasamehe ninyi kwa hiari kupitia Kristo.+
5 Kwa hiyo, iweni waigaji wa Mungu,+ kama watoto wapendwa, 2 na mwendelee kutembea katika upendo,+ kama vile Kristo pia alivyotupenda sisi*+ na kujitoa mwenyewe kwa ajili yetu* kuwa toleo na dhabihu yenye harufu tamu kwa Mungu.+
3 Uasherati* na kila namna ya ukosefu wa usafi au pupa visitajwe kamwe miongoni mwenu,+ kama inavyowafaa watu watakatifu;+ 4 wala mwenendo wa aibu wala maneno ya kipumbavu wala mizaha michafu+—mambo yasiyofaa—badala yake, kutoa shukrani.+ 5 Kwa maana mnajua hili, nanyi mnalitambua wenyewe, kwamba hakuna mwasherati*+ au mtu asiye safi au mtu mwenye pupa,+ maana yake mtu anayeabudu sanamu, aliye na urithi wowote katika Ufalme wa Kristo na wa Mungu.+
6 Mtu yeyote asiwadanganye kwa maneno matupu, kwa maana ghadhabu ya Mungu inakuja juu ya wana wa kutotii kwa sababu ya mambo hayo. 7 Kwa hiyo, msishirikiane nao; 8 kwa kuwa wakati fulani mlikuwa giza, lakini sasa ninyi ni nuru+ kuhusiana na Bwana.+ Endeleeni kutembea kama watoto wa nuru, 9 kwa maana tunda la nuru lina kila namna ya wema na uadilifu na kweli.+ 10 Endeleeni kuhakikisha jambo linalokubalika+ kwa Bwana; 11 na mwache kushiriki katika matendo yasiyozaa matunda, ambayo ni ya giza;+ badala yake, myafunue jinsi yalivyo. 12 Kwa maana mambo wanayotenda katika siri ni aibu hata kuyataja. 13 Basi mambo yote yanayofunuliwa yanawekwa wazi* na nuru, kwa maana kila jambo linalowekwa wazi ni nuru. 14 Kwa hiyo, inasemwa: “Amka, wewe unayelala usingizi, na ufufuke kutoka kwa wafu,+ na Kristo atakuangazia.”+
15 Basi endeleeni kuangalia sana jinsi mnavyotembea, si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, 16 mkiutumia vizuri kabisa wakati wenu,*+ kwa sababu siku hizi ni zenye uovu. 17 Kwa hiyo acheni kuwa watu wasio na akili, bali endeleeni kuyafahamu mapenzi ya Yehova.*+ 18 Pia, msilewe divai,+ ambayo ina upotovu,* bali endeleeni kujazwa roho. 19 Mkizungumza kati yenu* kwa zaburi, sifa kwa Mungu, na nyimbo za kiroho, mkiimba+ na kupiga muziki+ katika mioyo yenu kwa Yehova,*+ 20 sikuzote mkimtolea shukrani+ Mungu na Baba yetu kwa ajili ya mambo yote katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo.+
21 Jitiisheni kila mmoja kwa mwenzake+ katika kumwogopa Kristo. 22 Wake na wajitiishe kwa waume zao+ kama kwa Bwana, 23 kwa sababu mume ni kichwa cha mke wake+ kama vile Kristo alivyo kichwa cha kutaniko,+ yeye akiwa mwokozi wa mwili huu. 24 Kwa kweli, kama vile kutaniko linavyojitiisha kwa Kristo, wanawake pia wanapaswa kujitiisha kwa waume zao katika mambo yote. 25 Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu,+ kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake,+ 26 ili alitakase, akilisafisha na kuliosha kwa maji kupitia neno,+ 27 ili kujipa mwenyewe kutaniko likiwa na fahari, bila doa au kunyanzi au lolote kati ya mambo hayo,+ bali likiwa takatifu na bila dosari.+
28 Vivyo hivyo, waume wanapaswa kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Mwanamume anayempenda mke wake anajipenda mwenyewe, 29 kwa maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake, bali huulisha na kuutunza, kama vile Kristo anavyolitendea kutaniko, 30 kwa kuwa sisi ni viungo vya mwili wake.+ 31 “Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana* na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja.”+ 32 Siri hii takatifu+ ni kubwa. Sasa ninazungumza kuhusu Kristo na kutaniko.+ 33 Hata hivyo, kila mtu kati yenu anapaswa kumpenda mke wake+ kama anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.+
6 Enyi watoto, watiini wazazi wenu+ katika muungano na Bwana, kwa maana hilo ni jambo la uadilifu. 2 “Mheshimu baba yako na mama yako,”+ hiyo ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi: 3 “Ili mambo yakuendee vema* nawe ukae muda mrefu duniani.” 4 Nanyi akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu,+ bali endeleeni kuwalea katika nidhamu+ na maagizo ya* Yehova.*+
5 Enyi watumwa, watiini mabwana wenu wanadamu,*+ kwa kuogopa na kutetemeka kwa unyoofu wa mioyo yenu, kama vile kwa Kristo, 6 si wakati tu mnapotazamwa, ili tu kuwapendeza wanadamu,*+ bali kama watumwa wa Kristo mkifanya mapenzi ya Mungu kwa nafsi* yote.+ 7 Tumikieni mkiwa na mtazamo mzuri, kama kwa Yehova,*+ na si kwa wanadamu, 8 kwa maana mnajua kwamba wema wowote ambao kila mtu hufanya, Yehova* atamlipa wema huo,+ iwe ni mtumwa au mtu huru. 9 Pia, enyi mabwana, endeleeni kuwatendea kwa njia hiyohiyo, bila kuwatisha, kwa maana mnajua kwamba Bwana wao na wenu pia yuko mbinguni,+ naye hana ubaguzi wowote.
10 Mwishowe, endeleeni kujipatia nguvu+ katika Bwana na katika uwezo wa nguvu zake. 11 Vaeni mavazi kamili ya silaha+ kutoka kwa Mungu ili mweze kusimama imara dhidi ya matendo yenye hila ya* Ibilisi; 12 kwa sababu tunapambana,*+ si dhidi ya damu na mwili, bali dhidi ya serikali, dhidi ya mamlaka, dhidi ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, dhidi ya majeshi ya roho waovu+ katika mahali pa kimbingu. 13 Kwa sababu hiyo chukueni mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu,+ ili mweze kupinga katika ile siku ya uovu, na baada ya kutimiza mambo yote, mweze kusimama imara.
14 Kwa hiyo, simameni imara, mkiwa mmejifunga kiunoni mshipi wa ile kweli,+ mkiwa mmevaa bamba la kifuani la uadilifu,+ 15 na mkiwa mmevaa viatu miguuni tayari kutangaza habari njema ya amani.+ 16 Mbali na mambo hayo, chukueni ngao kubwa ya imani,+ ambayo kwa kuitumia mtaizima mishale yote inayowaka moto* ya yule mwovu.+ 17 Pia, pokeeni kofia ya chuma ya wokovu,+ na upanga wa roho, yaani, neno la Mungu,+ 18 na kwa kila namna ya sala+ na dua mkiendelea kusali kila wakati katika roho.+ Na hivyo kaeni macho, daima mkiomba dua kwa ajili ya watakatifu wote. 19 Pia, msali kwa ajili yangu, kwamba ninapofungua kinywa changu nipewe maneno, ili niweze kuzungumza kwa ujasiri ninapojulisha siri takatifu ya habari njema,+ 20 ambayo kwa ajili yake ninatenda kama balozi+ aliyefungwa minyororo, na kwamba niweze kuzungumza kuihusu kwa ujasiri, kama ninavyopaswa kuzungumza.
21 Basi ili ninyi pia mjue kunihusu na jinsi ninavyoendelea, Tikiko,+ ndugu mpendwa na mhudumu mwaminifu katika Bwana, atawajulisha mambo yote.+ 22 Ninamtuma kwenu kwa kusudi hili, ili mjue jinsi tunavyoendelea na aifariji mioyo yenu.
23 Akina ndugu na wawe na amani na upendo pamoja na imani kutoka kwa Mungu Baba na Bwana Yesu Kristo. 24 Fadhili zisizostahiliwa na ziwe pamoja na wote wanaompenda Bwana wetu Yesu Kristo katika hali ya kutoharibika.
Yaani, pamoja na Kristo.
Au “akili nzuri.”
Au “kusimamia mambo.”
Au “malipo ya awali; uthibitisho (dhamana) wa kile kitakachokuja.”
Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Au “mwenendo.”
Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Au “kibali chake.”
Au “matokeo ya kazi.”
Angalia Kamusi.
Angalia Nyongeza A5.
Au “unyenyekevu wa akili.”
Au “wahubiri wa habari njema.”
Au “kuwazoeza.”
Au “muungano.”
Tnn., “kukosa hisia katika.”
Au “ufidhuli; matendo ya kuchukiza yanayofanywa bila aibu.” Kigiriki, a·selʹgei·a. Angalia Kamusi.
Au “nguvu zinazotawala akili zenu.” Tnn., “roho ya akili yenu.”
Au labda, “ninyi.”
Au labda, “yenu.”
Neno la Kigiriki porneiʹa. Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi, “Uasherati.”
Au “yanakaripiwa.”
Tnn., “mkijinunulia wakati uliowekwa.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “haina adabu.”
Au labda, “mkijizungumzia.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “atabaki.”
Au “Ili ufanikiwe.”
Au “mwelekezo wa; mwongozo wa.” Tnn., “kuweka katika akili.”
Angalia Nyongeza A5.
Tnn., “wa kimwili.”
Tnn., “si kwa njia ya utumishi wa macho ili kuwapendeza wanadamu.”
Angalia Kamusi, “Nafsi.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Au “njama za.”
Tnn., “tunapigana mweleka.”
Au “makombora.”