BARUA YA PILI KWA WAKORINTHO
1 Paulo, mtume wa Kristo Yesu kupitia mapenzi ya Mungu, na Timotheo+ ndugu yetu, kwa kutaniko la Mungu lililo huko Korintho, pamoja na watakatifu wote walio katika Akaya yote:+
2 Na muwe na fadhili zisizostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo.
3 Asifiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo,+ Baba wa rehema nyororo+ na Mungu wa faraja yote,+ 4 ambaye hutufariji* katika majaribu*+ yetu yote, ili tuweze kuwafariji wengine+ walio katika majaribu* ya namna yoyote, kwa faraja ambayo tunapokea kutoka kwa Mungu.+ 5 Kwa maana kama vile mateso kwa ajili ya Kristo yalivyo mengi ndani yetu,+ ndivyo pia faraja tunayopokea kupitia Kristo ilivyo nyingi. 6 Basi tukikabili majaribu,* ni kwa ajili ya faraja na wokovu wenu; na tukifarijiwa, ni kwa ajili ya faraja yenu inayotenda ili kuwasaidia mvumilie mateso yaleyale ambayo sisi pia tunateseka. 7 Na tumaini letu kwa ajili yenu haliyumbi-yumbi, kwa kuwa tunajua kwamba kama vile mnavyoshiriki katika mateso, ndivyo pia mtakavyoshiriki katika faraja.+
8 Kwa maana hatutaki mkose kujua, akina ndugu, kuhusu dhiki tuliyopata katika mkoa wa Asia.+ Tulikuwa na mkazo mkubwa sana unaozidi nguvu zetu wenyewe, hivi kwamba hatukuwa na uhakika hata kuhusu uhai wetu.+ 9 Kwa kweli, tulihisi kwamba tumepokea hukumu ya kifo. Ilikuwa hivyo ili tusijitegemee sisi wenyewe, bali tumtegemee Mungu+ ambaye huwafufua wafu. 10 Alituokoa kutoka katika hatari kubwa ya kifo na atatuokoa, nasi tumeweka tumaini letu kwake kwamba ataendelea kutuokoa.+ 11 Ninyi pia mnaweza kutusaidia kwa kutoa dua kwa ajili yetu,+ ili wengi watoe shukrani kwa ajili yetu kwa kibali tunachopokea kwa sababu ya majibu ya sala za wengi.*+
12 Kwa maana hili ndilo jambo tunalojisifia, dhamiri yetu inatoa ushahidi kwamba tumejiendesha katika ulimwengu, na hasa kuwaelekea ninyi, kwa utakatifu na unyoofu unaotoka kwa Mungu, si kwa hekima ya kimwili,+ bali kwa fadhili zisizostahiliwa za Mungu. 13 Kwa maana kwa kweli hatuwaandikii jambo lolote isipokuwa yale mnayoweza kusoma* na kuyaelewa, nami natumaini mtaendelea kuyaelewa mambo haya kikamili,* 14 kama vile ambavyo pia mmeelewa kwa kadiri fulani, kwamba sisi ni sababu yenu ya kujisifu, kama vile mtakavyokuwa kwetu pia katika siku ya Bwana wetu Yesu.
15 Basi nikiwa na uhakika huu, nilikusudia kuja kwenu kwanza, ili muwe na pindi ya pili ya kuwa na shangwe;* 16 kwa maana nilikusudia kuwatembelea nikiwa safarini kwenda Makedonia, nirudi kwenu baada ya kutoka Makedonia, kisha mnisindikize kwenda Yudea.+ 17 Basi, nilipokusudia hivyo, je, nilipuuza jambo hilo? Au je, mimi ninakusudia mambo kwa njia ya kimwili hivi kwamba ninasema “Ndiyo, ndiyo” na kisha “Siyo, siyo”? 18 Lakini Mungu anaweza kutegemewa ili kwamba yale tunayowaambia yasiwe “ndiyo” na wakati uleule “siyo.” 19 Kwa maana Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, aliyehubiriwa miongoni mwenu kupitia sisi, yaani, kupitia mimi na Silvano* na Timotheo,+ hakuwa “ndiyo” na wakati uleule “siyo,” bali kuhusiana naye “ndiyo” imekuwa “ndiyo.” 20 Kwa maana hata ahadi za Mungu ziwe nyingi kadiri gani, zimekuwa “ndiyo” kupitia yeye.+ Kwa hiyo, kupitia yeye pia “Amina” husemwa kwa Mungu,+ nayo humletea utukufu kupitia sisi. 21 Lakini yule anayetoa uhakikisho kwamba ninyi na sisi ni wa Kristo na yule ambaye ametutia mafuta ni Mungu.+ 22 Yeye pia ametia muhuri wake juu yetu+ naye ametupatia rehani ya kile kitakachokuja,* yaani, roho,+ katika mioyo yetu.
23 Sasa ninamwita Mungu awe shahidi dhidi yangu,* kwamba sijaja Korintho kwa sababu ya kuwahurumia ninyi. 24 Si kwamba sisi ni mabwana wa imani yenu,+ bali sisi ni wafanyakazi wenzenu kwa ajili ya shangwe yenu, kwa maana mnasimama kwa imani yenu.
2 Kwa maana nimeamua kwamba sitakuja kwenu tena kwa huzuni. 2 Kwa maana nikiwahuzunisha ninyi, ni nani atakayekuwapo ili kunichangamsha isipokuwa yule ambaye nilimhuzunisha? 3 Niliandika mambo hayo, ili, nitakapokuja, nisihuzunishwe na wale ambao ninapaswa kushangilia juu yao, kwa sababu nina uhakika kwamba kile kinachonipa shangwe kinawapa ninyi nyote shangwe hiyohiyo. 4 Kwa maana kutokana na dhiki nyingi na maumivu ya moyo niliwaandikia kwa machozi mengi, si ili niwahuzunishe,+ bali niwajulishe kina cha upendo wangu kwenu.
5 Basi ikiwa yeyote amesababisha huzuni,+ hajanihuzunisha mimi, bali amewahuzunisha ninyi nyote kwa kadiri fulani—nisiwe mkali mno kwa yale ninayosema. 6 Karipio hili linalotolewa na wengi linamtosha mtu huyo; 7 badala yake, sasa mnapaswa kumsamehe kwa fadhili na kumfariji,+ ili asilemewe* na huzuni inayopita kiasi.+ 8 Kwa hiyo ninawahimiza ninyi kumthibitishia upendo wenu.+ 9 Ndiyo sababu niliwaandikia pia: ili kujua kama mngeonyesha uthibitisho wa utii wenu katika mambo yote. 10 Mkimsamehe mtu yeyote jambo lolote, mimi pia ninamsamehe. Kwa kweli, lolote ambalo nimesamehe (ikiwa nimesamehe jambo lolote) ni kwa ajili yenu machoni pa Kristo, 11 ili Shetani asitushinde akili,*+ kwa maana hatukosi kuzijua mbinu* zake.+
12 Basi nilipofika Troa+ kutangaza habari njema kuhusu Kristo nami nikafunguliwa mlango katika Bwana, 13 roho yangu haikupata kitulizo kwa sababu sikumkuta Tito+ ndugu yangu. Basi, nikawaaga kisha nikaondoka kwenda Makedonia.+
14 Lakini shukrani kwa Mungu, ambaye sikuzote hutuongoza katika maandamano ya ushindi kwa kushirikiana na Kristo, na kupitia sisi huieneza* harufu nzuri ya ujuzi kumhusu kila mahali! 15 Kwa maana kwa Mungu sisi ni harufu tamu ya Kristo kati ya wale wanaookolewa na kati ya wale wanaoangamia; 16 kwa hawa wa mwisho ni harufu ya kifo inayoleta kifo,+ kwa wale wa kwanza ni harufu ya uzima inayoleta uzima. Na ni nani anayestahili kabisa mambo haya? 17 Ni sisi, kwa maana sisi si wachuuzi wa* neno la Mungu+ kama watu wengi walivyo, bali tunasema kwa unyoofu wote, tukiwa tumetumwa na Mungu, ndiyo, machoni pa Mungu na kwa kushirikiana na Kristo.
3 Je, tunaanza tena kujipendekeza wenyewe? Au kama watu fulani, je, tunahitaji barua za pendekezo kuja au kutoka kwenu? 2 Ninyi wenyewe ndio barua yetu,+ iliyoandikwa juu ya mioyo yetu na kujulikana na kusomwa na wanadamu wote. 3 Kwa maana ni wazi kwamba ninyi ni barua ya Kristo ambayo tuliandika tukiwa wahudumu,+ iliyoandikwa si kwa wino bali kwa roho ya Mungu aliye hai, si juu ya mabamba ya mawe,+ bali juu ya mabamba ya nyama, juu ya mioyo.+
4 Tuna uhakika wa namna hii kwa Mungu kupitia Kristo. 5 Si kwamba sisi wenyewe tunastahili vya kutosha kufikiri kuwa jambo lolote linatoka kwetu, bali kustahili kwetu vya kutosha hutoka kwa Mungu,+ 6 ambaye kwa kweli ametustahilisha vya kutosha kuwa wahudumu wa agano jipya,+ si wa sheria zilizoandikwa,+ bali wa roho; kwa maana sheria zilizoandikwa huleta hukumu ya kifo,+ bali roho hufanya kuwa hai.+
7 Basi ikiwa sheria zinazotoa kifo ambazo zilichongwa kwa herufi kwenye mawe+ zilikuja kwa utukufu kama huo hivi kwamba wana wa Israeli hawakuweza kuutazama uso wa Musa kwa sababu ya utukufu wa uso wake,+ utukufu ambao ungekuja kuondolewa, 8 kwa nini kutolewa kwa roho+ kusiwe kwenye utukufu zaidi?+ 9 Kwa maana ikiwa sheria zilizotoa hukumu ya hatia+ zilikuwa zenye utukufu,+ kutolewa kwa uadilifu kungekuwa na utukufu mwingi kadiri gani!+ 10 Kwa kweli, hata kile ambacho wakati fulani kilifanywa kiwe na utukufu kimevuliwa utukufu, kwa sababu ya utukufu unaokizidi.+ 11 Kwa maana ikiwa kile ambacho kingeondolewa kiliingizwa kwa utukufu,+ basi utukufu wa kinachobaki ungekuwa mwingi kadiri gani!+
12 Kwa kuwa tuna tumaini hilo,+ tunazungumza kwa uhuru mwingi, 13 nasi hatufanyi kama Musa alivyofanya alipofunika uso wake kwa kitambaa+ ili wana wa Israeli wasitazame mwisho wa kile ambacho kingeondolewa. 14 Lakini akili zao zilitiwa uzito.+ Kwa maana mpaka leo kitambaa kilekile kinadumu bila kuondolewa agano la zamani linaposomwa,+ kwa sababu kinaondolewa tu kupitia Kristo.+ 15 Kwa kweli, mpaka leo kila mara maandishi ya Musa yanaposomwa,+ kitambaa hukaa juu ya mioyo yao.+ 16 Lakini mtu anapomgeukia Yehova,* kitambaa huondolewa.+ 17 Basi Yehova* ni Roho,+ na mahali palipo na roho ya Yehova,* pana uhuru.+ 18 Na sisi sote, tunapotoa kama vioo mrudisho wa utukufu wa Yehova* tukiwa na nyuso zisizo na kitambaa, tunageuzwa kuwa katika mfano uleule kutoka kiwango kimoja cha utukufu mpaka kingine,* sawa na anavyofanya Yehova* ambaye ni Roho.*+
4 Kwa hiyo, kwa kuwa tuna huduma hii kupitia rehema tuliyoonyeshwa, hatufi moyo. 2 Hata hivyo, tumeyakataa mambo ya kichinichini ya aibu, hatutembei kwa ujanja, au kulichanganya na kitu chochote neno la Mungu;+ bali kwa kufanya kweli iwe wazi, tunajipendekeza kwa kila dhamiri ya mwanadamu machoni pa Mungu.+ 3 Ikiwa kwa kweli habari njema tunayotangaza imefunikwa kwa kitambaa, imefunikwa kati ya wale wanaoangamia, 4 ambao kati yao mungu wa mfumo huu wa mambo*+ amezipofusha akili za wasioamini,+ ili nuru ya* habari njema yenye utukufu kuhusu Kristo, aliye mfano wa Mungu,+ isiwaangazie.+ 5 Kwa maana tunahubiri, si kuhusu sisi wenyewe, bali kuhusu Yesu Kristo kwamba ni Bwana na sisi wenyewe kwamba ni watumwa wenu kwa ajili ya Yesu. 6 Kwa maana Mungu ndiye aliyesema: “Nuru na iangaze kutoka katika giza,”+ naye ameangaza juu ya mioyo yetu ili kuimulika+ kwa ujuzi wenye utukufu kumhusu Mungu kupitia uso wa Kristo.
7 Hata hivyo, tuna hazina hii+ katika vyombo vya udongo,*+ ili nguvu zinazopita zile za kawaida ziwe za Mungu na si kutoka kwetu.+ 8 Tunakandamizwa katika kila njia, lakini hatubanwi kupita kiasi cha kushindwa kusonga; tunafadhaishwa, lakini si bila njia ya kutokea kabisa;*+ 9 tunateswa, lakini hatuachwi bila msaada;+ tunaangushwa chini, lakini hatuangamizwi.+ 10 Sikuzote katika mwili wetu tunavumilia matendo yenye kuleta kifo ambayo Yesu aliteseka,+ ili uzima wa Yesu ufunuliwe pia katika mwili wetu. 11 Kwa maana sikuzote sisi tunaoishi tunakabili kifo uso kwa uso+ kwa ajili ya Yesu, ili uzima wa Yesu ufunuliwe pia katika mwili wetu unaoweza kufa. 12 Kwa hiyo kifo kinafanya kazi ndani yetu, lakini uzima ndani yenu.
13 Basi kwa sababu tuna roho ileile ya imani kama ile iliyoandikwa hivi kuihusu: “Mimi nilionyesha imani, kwa hiyo nikasema”;+ sisi pia tunaonyesha imani na kwa hiyo tunasema, 14 tukijua kwamba Yule aliyemfufua Yesu atatufufua sisi pia pamoja na Yesu naye atatutokeza sisi pamoja nanyi.+ 15 Kwa maana mambo yote haya ni kwa ajili yenu, ili fadhili zisizostahiliwa zinazoongezeka zizidi kuwa nyingi kwa sababu wengi zaidi wanatoa shukrani kwa utukufu wa Mungu.+
16 Kwa hiyo, hatufi moyo, lakini hata ikiwa mtu tuliye kwa nje anachakaa, hakika mtu tuliye kwa ndani anafanywa upya siku kwa siku. 17 Kwa maana ingawa dhiki* ni ya muda mfupi na ni nyepesi, inatokeza kwa ajili yetu utukufu ulio mkuu* na bora zaidi na zaidi, na wa milele;+ 18 huku tukikaza macho yetu, si juu ya vitu vinavyoonekana, bali juu ya vitu visivyoonekana.+ Kwa maana vitu vinavyoonekana ni vya muda, lakini vitu visivyoonekana ni vya milele.
5 Kwa maana tunajua kwamba nyumba yetu ya kidunia, hema hili, likiharibiwa,*+ tutapata jengo kutoka kwa Mungu, nyumba ya milele mbinguni, ambayo haijajengwa kwa mikono.+ 2 Kwa maana tunaugua kwelikweli katika nyumba hii,* tukitamani sana kuvaa ile yetu* kutoka mbinguni,*+ 3 ili kwamba tutakapoivaa, hatutapatikana tukiwa uchi. 4 Kwa kweli, sisi tulio katika hema hili tunaugua, tukilemewa kwa sababu hatutaki kuuvua huu, bali tunataka kuuvaa ule mwingine,+ ili uhai ukimeze kile kinachoweza kufa.+ 5 Basi yule aliyetutayarisha kwa ajili ya jambo hili ni Mungu,+ ambaye alitupatia roho kama rehani ya kile kitakachokuja.*+
6 Basi sikuzote sisi tuna uhodari mwingi na tunajua kwamba tukiwa na makao yetu katika mwili, hatupo mahali alipo Bwana,+ 7 kwa maana tunatembea kwa imani, si kwa kuona. 8 Lakini sisi tuna uhodari mwingi na tungependelea tusiwepo katika mwili bali tuyafanye makao yetu pamoja na Bwana.+ 9 Basi iwe ni nyumbani pamoja naye au tusipokuwa pamoja naye, lengo letu ni kukubalika kwake. 10 Kwa maana lazima sisi sote tusimame* mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo, ili kila mmoja apate malipo kulingana na mambo aliyotenda akiwa katika mwili, yawe mema au mabaya.*+
11 Kwa hiyo, kwa kuwa tunajua kumwogopa Bwana, tunaendelea kuwashawishi watu, lakini tunafahamika vizuri* kwa Mungu. Hata hivyo, ninatumaini kwamba tunafahamika vizuri* pia kwa dhamiri zenu. 12 Hatujipendekezi wenyewe tena kwenu, bali tunawapa kichocheo cha kujisifu kuhusiana nasi, ili muweze kujibu wale wanaojisifu kuhusu sura ya nje+ bali si kuhusu yaliyo moyoni. 13 Kwa maana ikiwa tulikuwa tumerukwa na akili,+ ilikuwa ni kwa ajili ya Mungu; ikiwa tuna akili timamu, ni kwa ajili yenu. 14 Kwa maana upendo alio nao Kristo hutuchochea, kwa sababu tumefikia uamuzi huu, kwamba mtu mmoja alikufa kwa ajili ya wote;+ hivyo basi, wote walikuwa wamekufa. 15 Naye alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe,+ bali kwa ajili ya yule aliyekufa kwa ajili yao na kufufuliwa.
16 Basi tangu sasa hatumjui mtu yeyote kulingana na maoni ya kimwili.+ Hata kama wakati fulani tulimjua Kristo kulingana na mwili, kwa hakika hatumjui tena kwa njia hiyo.+ 17 Kwa hiyo, ikiwa yeyote yuko katika muungano na Kristo, yeye ni kiumbe kipya;+ mambo ya zamani yalipitilia mbali; tazama! mambo mapya yamekuja kuwapo. 18 Lakini mambo yote yametoka kwa Mungu, aliyetupatanisha sisi kwake mwenyewe kupitia Kristo+ na kutupatia huduma ya upatanisho,+ 19 yaani, kwamba Mungu kupitia Kristo alikuwa akiupatanisha ulimwengu kwake mwenyewe,+ bila kuwahesabia makosa yao,+ naye alitukabidhi ujumbe wa upatanisho.+
20 Kwa hiyo sisi ni mabalozi+ walio badala ya Kristo,+ kana kwamba Mungu alikuwa akisihi kupitia sisi. Kama walio badala ya Kristo, tunaomba: “Mpatanishwe na Mungu.” 21 Yule ambaye hakujua dhambi+ alimfanya kuwa dhambi* kwa ajili yetu, ili kupitia yeye tuwe uadilifu wa Mungu.+
6 Huku tukifanya kazi pamoja naye,+ tunawahimiza pia msipokee fadhili zisizostahiliwa za Mungu na kukosa kusudi lake.+ 2 Kwa maana anasema: “Katika wakati unaokubalika nilikusikia, na katika siku ya wokovu nilikusaidia.”+ Tazama! Sasa ndio wakati unaokubalika hasa. Tazama! Sasa ndiyo siku ya wokovu.
3 Hatutoi sababu yoyote ya kukwaza, ili kosa lolote lisipatikane katika huduma yetu;+ 4 bali katika kila njia tunajipendekeza kuwa wahudumu wa Mungu,+ kwa kuvumilia mengi, kwa dhiki, kwa nyakati za uhitaji, kwa shida,+ 5 kwa kupigwa, kwa kufungwa gerezani,+ kwa machafuko, kwa kazi ngumu, kwa kukosa usingizi usiku, kwa nyakati za kukosa chakula;+ 6 kwa utakaso, kwa ujuzi, kwa subira,+ kwa fadhili,+ kwa roho takatifu, kwa upendo usio na unafiki,+ 7 kwa kusema maneno ya kweli, kwa nguvu za Mungu;+ kupitia silaha za uadilifu+ katika mkono wa kulia* na wa kushoto,* 8 kupitia utukufu na aibu, kupitia habari mbaya na habari nzuri. Tunaonwa kuwa wadanganyifu na bado tunasema ukweli, 9 kama wasiojulikana na bado tunatambuliwa, kama wanaokufa* na bado, tazama! tunaishi,+ kama walioadhibiwa* na bado hatujakabidhiwa kwenye kifo,+ 10 kama walio na huzuni lakini wanaoshangilia sikuzote, kama maskini lakini wanaowatajirisha wengi, kama wasio na kitu chochote na bado walio na vitu vyote.+
11 Tumefungua kinywa chetu ili kuzungumza* nanyi, enyi Wakorintho, nasi tumefungua wazi moyo wetu. 12 Hatujajizuia* kuwaonyesha upendo,+ bali ninyi mmejizuia kutuonyesha upendo wenu mwororo. 13 Kwa hiyo, kwa kujibu—ninazungumza kama na watoto wangu—ninyi pia fungueni kabisa mioyo yenu.*+
14 Msifungwe nira* isivyo sawa pamoja na wasio waamini.+ Kwa maana kuna ushirika gani kati ya uadilifu na uasi sheria?+ Au nuru ina ushirika gani na giza?+ 15 Isitoshe, kuna upatano gani kati ya Kristo na Beliali?*+ Au mwamini* ana ushirika gani* na mtu asiye mwamini?+ 16 Na hekalu la Mungu lina makubaliano gani na sanamu?+ Kwa maana sisi ni hekalu la Mungu aliye hai;+ kama Mungu alivyosema: “Mimi nitakaa miongoni mwao+ na kutembea miongoni mwao, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.”+ 17 “‘Kwa hiyo, tokeni miongoni mwao na mjitenge,’ asema Yehova,* ‘na mwache kugusa kitu kichafu’”;+ “‘nami nitawakaribisha ndani.’”+ 18 “‘Nami nitakuwa baba kwenu,+ nanyi mtakuwa wana na mabinti kwangu,’+ asema Yehova,* Mweza Yote.”
7 Kwa hiyo, wapendwa, kwa kuwa tuna ahadi hizi,+ acheni tujisafishe kila unajisi wa mwili na roho,+ tukiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.
2 Tupatieni nafasi mioyoni mwenu.+ Hatujamkosea yeyote, hatujamharibu yeyote, hatujamdanganya yeyote ili tupate faida.+ 3 Sisemi jambo hili ili niwahukumu. Kwa maana tayari nimesema kwamba ninyi mko ndani ya mioyo yetu ili kufa pamoja na kuishi pamoja. 4 Nina uhuru mwingi wa kusema kuwaelekea ninyi. Ninajisifu sana kuhusiana nanyi. Nimejawa na faraja; ninafurika shangwe katika taabu yetu yote.+
5 Kwa kweli, tulipofika Makedonia,+ miili yetu haikupata kitulizo, bali tuliendelea kutaabishwa katika kila njia—nje kulikuwa na mapigano na ndani woga. 6 Lakini Mungu, ambaye huwafariji wale waliovunjika moyo,+ alitufariji kwa kuwapo kwa Tito; 7 na si kwa kuwapo kwake tu bali pia kwa faraja ambayo alipokea kwa sababu yenu, kwa kuwa alirudi na kutujulisha kuhusu tamaa yenu ya kuniona, huzuni yenu nyingi, na jinsi mlivyonihangaikia sana;* hivyo nikashangilia hata zaidi.
8 Kwa maana hata kama niliwahuzunisha kwa barua yangu,+ sijuti kuhusu jambo hilo. Ingawa mwanzoni nilijuta (nilipoona kwamba barua hiyo iliwahuzunisha, ingawa ni kwa muda mfupi tu), 9 sasa ninashangilia, si kwa sababu mlihuzunishwa tu, bali kwa sababu mlihuzunishwa hivi kwamba mkatubu. Kwa maana mlihuzunishwa kwa njia ya kimungu, kwa hiyo hamkupata madhara kwa sababu yetu. 10 Kwa kuwa huzuni kwa njia ya kimungu hutokeza toba inayoongoza kwenye wokovu, bila kuleta majuto;+ lakini huzuni ya ulimwengu hutokeza kifo. 11 Kwa maana, ona jinsi kuhuzunishwa kwenu kwa njia ya kimungu kulivyotokeza bidii nyingi ndani yenu, ndiyo, mlijiondolea hatia, ndiyo, ghadhabu, ndiyo, woga, ndiyo, kutamani sana,* ndiyo, bidii, ndiyo, kurekebisha kosa!+ Katika kila njia mlijionyesha kuwa safi* kuhusu jambo hili. 12 Ingawa niliwaandikia, sikufanya hivyo kwa ajili ya yule aliyefanya kosa,+ wala kwa ajili ya yule aliyekosewa, bali ili bidii yenu kwa ajili yetu ithibitishwe miongoni mwenu machoni pa Mungu. 13 Ndiyo sababu tumefarijiwa.
Lakini kwa kuongezea faraja yetu, tulishangilia hata zaidi kuhusu shangwe ya Tito, kwa sababu ninyi nyote mliiburudisha roho yake. 14 Kwa maana ikiwa nimejisifu kwake juu yenu, sijapata aibu; lakini kama vile mambo tuliyowaambia yalivyokuwa ya kweli, ndivyo pia kujisifu kwetu kwa Tito kumekuwa kweli. 15 Pia, upendo wake mwororo kwenu ni mwingi anapokumbuka utii wenu nyote,+ jinsi mlivyompokea kwa kuogopa na kutetemeka. 16 Ninashangilia kwamba katika kila njia nitakuwa na uhakika kuwahusu ninyi.*
8 Basi akina ndugu, tunawajulisha kuhusu fadhili zisizostahiliwa za Mungu ambazo makutaniko ya Makedonia+ yamepewa. 2 Wakati wa majaribu makali chini ya mateso, shangwe yao nyingi na umaskini mkubwa ulifanya utajiri wa ukarimu wao uwe mwingi.* 3 Kwa maana ilikuwa kulingana na uwezo wao,+ ndiyo, ninashuhudia, hata kupita uwezo wao,+ 4 nao kwa kupenda kwao wenyewe waliendelea kutuomba sana wapate pendeleo la kutoa kwa fadhili, ili washiriki katika huduma ya kutoa msaada kwa ajili ya watakatifu.+ 5 Na si kama tulivyotumaini tu, bali kwanza walijitoa wenyewe kwa Bwana na kwetu kupitia mapenzi ya Mungu. 6 Basi tukamtia moyo Tito+ kwamba kama vile alivyokuwa ameanzisha kazi hii kati yenu, pia akamilishe utoaji huu wenye fadhili kwa upande wenu. 7 Hata hivyo, kama vile mlivyo na utajiri katika kila jambo, katika imani na neno na ujuzi na bidii yote na katika upendo wetu kwenu, pia mzidi katika utoaji huu wenye fadhili.+
8 Sisemi hivi ili kuwaamuru, bali kuwajulisha kuhusu bidii ya wengine na kuujaribu uhalisi wa upendo wenu. 9 Kwa maana mnazijua fadhili zisizostahiliwa za Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba ingawa alikuwa tajiri, alikuja kuwa maskini kwa ajili yenu,+ ili muwe matajiri kupitia umaskini wake.
10 Kuhusu jambo hili ninatoa maoni yangu:+ Hii ni kwa ajili ya faida yenu, kwa kuwa tayari mwaka mmoja uliopita hamkuchukua tu hatua, bali pia mlionyesha tamaa ya kufanya hivyo. 11 Hivyo basi, malizeni pia kile mlichoanza kufanya, ili utayari wenu wa kutenda ukamilishwe kulingana na uwezo mlio nao. 12 Kwa maana ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika zaidi kulingana na kile ambacho mtu anacho,+ si kulingana na kile ambacho mtu hana. 13 Kwa maana sitaki kufanya iwe rahisi kwa wengine, lakini vigumu kwenu; 14 bali kwamba kupitia usawazisho, ziada yenu kwa sasa ijazie uhitaji wao, ili ziada yao pia ijazie upungufu wenu, ili kuwe na usawazisho. 15 Kama ilivyoandikwa: “Mtu aliyekuwa na vingi hakuwa na vingi mno, na mtu aliyekuwa na vichache hakuwa na vichache mno.”+
16 Basi shukrani kwa Mungu kwa kumfanya Tito awahangaikie ninyi kwa bidii ileile kutoka moyoni,+ 17 kwa sababu kwa kweli ameitikia tulipomtia moyo, lakini akiwa mwenye bidii sana, anakuja kwenu kwa kupenda kwake mwenyewe. 18 Lakini pamoja naye tunamtuma ndugu ambaye sifa yake kuhusiana na habari njema imeenea katika makutaniko yote. 19 Si hayo tu, bali pia makutaniko yalimweka rasmi asafiri pamoja nasi tunaposhughulikia zawadi hii ya fadhili kwa ajili ya utukufu wa Bwana na kwa uthibitisho wa utayari wetu wa kusaidia. 20 Hivyo, tunaepuka kulaumiwa na mtu yeyote kuhusiana na mchango huu wa ukarimu ambao tunaushughulikia.+ 21 Kwa maana ‘tunashughulikia mambo yote kwa unyoofu, si machoni pa Yehova* tu bali pia machoni pa wanadamu.’+
22 Zaidi ya hayo, pamoja nao tunamtuma ndugu yetu ambaye mara nyingi tumemjaribu na kuona ana bidii katika mambo mengi, lakini sasa ana bidii nyingi zaidi kwa sababu ya uhakika wake mkubwa kwenu. 23 Ingawa hivyo, kama kuna swali lolote kumhusu Tito, yeye ni mwenzangu* na mfanyakazi mwenzi kwa ajili ya faida yenu; au kama kuna swali kuhusu ndugu zetu, wao ni mitume wa makutaniko na utukufu wa Kristo. 24 Basi thibitisheni upendo wenu kwao,+ na mwonyeshe makutaniko sababu iliyofanya tujisifu kuwahusu ninyi.
9 Basi kuhusu huduma ambayo ni kwa ajili ya watakatifu,+ kwa kweli si lazima niwaandikie ninyi, 2 kwa maana ninajua utayari wenu ambao ninajisifia kwa Wamakedonia, kwamba Akaya imekuwa tayari kwa mwaka mmoja sasa, na bidii yenu imewachochea wengi kati yao. 3 Lakini ninawatuma akina ndugu, ili kujisifu kwetu juu yenu kusiwe bure kuhusiana na jambo hilo, na kwamba muwe tayari kwelikweli, kama nilivyosema mtakuwa. 4 La sivyo, Wamakedonia wakija pamoja nami na kukuta hamko tayari, sisi—nanyi pia—tutaona aibu kwa sababu ya uhakika wetu kwenu. 5 Basi niliona ni jambo muhimu kuwatia moyo akina ndugu watangulie kuja kwenu na kuitayarisha mapema zawadi yenu ya ukarimu iliyoahidiwa, ili iwe tayari kama zawadi ya ukarimu, bali si kama kitu cha kulazimishwa.
6 Lakini kuhusu hili, yeyote anayepanda kwa uhaba atavuna pia kwa uhaba, naye anayepanda kwa wingi atavuna pia kwa wingi.+ 7 Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda* wala kwa kulazimishwa,+ kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.+
8 Isitoshe, Mungu anaweza kufanya fadhili zake zote zisizostahiliwa ziwe nyingi kuwaelekea, ili sikuzote muwe na vitu vya kuwatosheleza kabisa katika kila jambo, na pia muwe na vingi kwa ajili ya kila kazi njema.+ 9 (Kama ilivyoandikwa: “Amegawa kwa wingi;* amewapa maskini. Uadilifu wake unadumu milele.”+ 10 Basi Yule ambaye humgawia mpandaji mbegu kwa wingi na mkate wa kula atawagawia na kuwazidishia ninyi mbegu ili mzipande naye ataongeza mavuno ya uadilifu wenu.) 11 Katika kila jambo mnatajirishwa kwa ajili ya kila namna ya ukarimu, ambao kupitia kwetu hufanya watu wamshukuru Mungu; 12 kwa kuwa huduma ya utumishi huu wa watu wote si kuandaa vizuri tu mahitaji ya watakatifu+ bali pia kuwe na utajiri wa shukrani nyingi kwa Mungu. 13 Kupitia uthibitisho wa huduma hii ya kutoa msaada, wanamtukuza Mungu kwa sababu mnajitiisha kwenye habari njema kumhusu Kristo, kama mlivyotangaza hadharani, na kwa sababu ninyi ni wakarimu katika mchango wenu kwao na kwa wote.+ 14 Na kupitia dua kwa ajili yenu, wanaonyesha upendo wao kwenu kwa sababu ya fadhili nyingi zisizostahiliwa za Mungu juu yenu.
15 Shukrani kwa Mungu kwa ajili ya zawadi yake ya bure isiyoelezeka.
10 Basi mimi mwenyewe, Paulo, ninawasihi kwa upole na fadhili za Kristo,+ ingawa mimi ni wa hali ya chini ninapokuwa kati yenu uso kwa uso,+ lakini jasiri kuwaelekea ninyi nisipokuwapo.+ 2 Ninaomba kwamba nitakapokuwapo, nisilazimike kuwa jasiri na kuchukua hatua kali ambazo ninakusudia dhidi ya wale wanaotuona kana kwamba tulitembea kwa njia ya kimwili. 3 Kwa maana ingawa tunatembea katika mwili, hatupigani vita kulingana na vile tulivyo katika mwili. 4 Kwa maana silaha za vita vyetu si za kimwili,+ bali ni zenye nguvu kupitia Mungu+ kwa ajili ya kuzipindua ngome zenye nguvu. 5 Kwa maana tunapindua mawazo na kila jambo lililo juu sana ambalo limeinuliwa kinyume cha ujuzi wa Mungu,+ nasi tunaiteka kila fikira ili kuifanya imtii Kristo; 6 nasi tuko tayari kutoa adhabu kwa ajili ya kila tendo la kutotii,+ mara tu utii wenu utakapokamilika.
7 Mnayatazama mambo kulingana na thamani yake ya nje. Mtu yeyote akijiamini kwamba yeye ni wa Kristo, acheni afikirie tena jambo hili: Kama vile yeye alivyo wa Kristo, ndivyo na sisi pia. 8 Kwa maana hata nikijisifu sana kuhusu mamlaka ambayo Bwana alitupatia ili tuwajenge wala si kuwabomoa ninyi,+ mimi sitaaibishwa. 9 Kwa maana sitaki ionekane kama ninajaribu kuwatisha kwa barua zangu. 10 Kwa maana wanasema: “Barua zake ni nzito na zenye nguvu, lakini akiwapo yeye mwenyewe, ni dhaifu na maneno yake ni yenye kudharaulika.” 11 Mtu kama huyo ajue kwamba mambo tunayosema* kupitia barua tusipokuwapo, tutayafanya pia* tutakapokuwapo.+ 12 Kwa maana sisi hatuthubutu kujiweka katika kikundi au kujilinganisha na watu fulani wanaojipendekeza wenyewe.+ Lakini wanapojipima wenyewe kwa wenyewe na kujilinganisha wenyewe kwa wenyewe, hawana uelewaji.+
13 Hata hivyo, hatutajisifu nje ya mipaka tuliyogawiwa, bali katika mpaka wa eneo ambalo Mungu alitupimia,* na kuufanya ufike hadi kwenu.+ 14 Kwa kweli, sisi hatuvuki mpaka wetu kana kwamba hatukuwafikia ninyi, kwa maana tulikuwa wa kwanza kufika hadi kwenu tukiwa na habari njema kuhusu Kristo.+ 15 Hapana, hatujisifu kuhusu kazi za mtu mwingine nje ya mipaka tuliyogawiwa, bali tunatumaini kwamba imani yenu inapozidi kuongezeka, mambo tuliyofanya yatazidi kuongezeka katika eneo letu. Ndipo tutazidi hata zaidi, 16 ili tutangaze habari njema katika nchi zilizo ng’ambo yenu, na hivyo tusijisifu kuhusu mambo ambayo tayari yamefanywa katika eneo la mtu mwingine. 17 “Lakini yule anayejisifu, na ajisifu katika Yehova.”*+ 18 Kwa maana si yule anayejipendekeza ambaye hukubaliwa,+ bali ni yule ambaye Yehova* humpendekeza.+
11 Laiti mngenivumilia katika kukosa kidogo akili. Lakini kwa kweli, mnanivumilia! 2 Kwa maana nina wivu juu yenu, wivu wa kimungu,* kwa kuwa mimi binafsi niliwachumbia mume mmoja ili niwatoe mkiwa bikira safi* kwa Kristo.+ 3 Lakini kwa njia fulani, ninaogopa kwamba kama nyoka alivyomshawishi Hawa kwa ujanja,+ huenda akili zenu zikapotoshwa kutoka kwenye unyoofu wa moyo na usafi* unaomfaa Kristo.+ 4 Kwa maana, kama ilivyo, mtu akija na kuhubiri Yesu mwingine tofauti na yule tuliyemhubiri, au mkipokea roho nyingine tofauti na ile mliyopokea,+ au habari njema nyingine tofauti na ile mliyokubali, mnakubaliana naye. 5 Kwa maana ninaona kwamba katika jambo lolote sijawa mdogo kuliko mitume wenu walio bora sana.+ 6 Lakini hata kama sina ustadi wa kusema,+ hakika nina ujuzi; kwa kweli tuliwafafanulia katika kila njia na katika mambo yote.
7 Au je, nilifanya dhambi kwa kujinyenyekeza ili ninyi mwinuliwe, kwa sababu niliwatangazia habari njema ya Mungu kwa furaha bila gharama?+ 8 Niliyanyang’anya* makutaniko mengine kwa kupokea vitu* kutoka kwao ili niwahudumie ninyi.+ 9 Na bado, nilipokuwa pamoja nanyi na nikapatwa na uhitaji, sikuwa mzigo kwa mtu yeyote, kwa maana ndugu waliotoka Makedonia walinipatia mahitaji yangu kwa wingi.+ Ndiyo, katika kila njia sikutaka kuwa mzigo kwenu nami nitaendelea kufanya hivyo.+ 10 Kwa hakika ikiwa kweli ya Kristo imo ndani yangu, sitaacha kujisifu+ katika maeneo ya Akaya. 11 Kwa sababu gani? Je, ni kwa sababu siwapendi? Mungu anajua ninawapenda.
12 Lakini nitaendelea kufanya kile ninachofanya,+ ili niondoe kisingizio cha wale wanaotafuta sababu ya kuonekana* kuwa sawa na sisi katika mambo ambayo* wanajisifia. 13 Kwa maana watu wa namna hiyo ni mitume wa uwongo, wafanyakazi wadanganyifu, wanaojifanya kuwa mitume wa Kristo.+ 14 Na si ajabu, kwa maana Shetani mwenyewe huendelea kujifanya kuwa malaika wa nuru.+ 15 Kwa hiyo si ajabu kwamba wahudumu wake pia huendelea kujifanya kuwa wahudumu wa uadilifu. Lakini mwisho wao utakuwa kulingana na matendo yao.+
16 Ninasema tena: Mtu yeyote asifikiri kwamba mimi sina akili. Lakini hata mkifikiri hivyo, basi mnikubali kama mtu asiye na akili, ili mimi pia nijisifu kidogo. 17 Hili ndilo ninalosema sasa, si kwa kufuata kielelezo cha Bwana, bali kama mtu asiye na akili, kwa ujasiri wa kujisifu. 18 Kwa kuwa wengi wanajisifu kulingana na mwili,* mimi pia nitajisifu. 19 Kwa kuwa ninyi mna “akili” sana, mnakubaliana kwa furaha na watu wasio na akili. 20 Kwa kweli, mnakubaliana na yeyote anayewafanya kuwa watumwa, yeyote anayemeza mali yenu, yeyote anayenyakua kile mlicho nacho, yeyote anayejitukuza juu yenu, na yeyote anayewapiga usoni.
21 Ninasema hili kwa aibu yetu, kwa sababu huenda ikaonekana tumetenda kwa udhaifu.
Lakini ikiwa wengine wanatenda kwa ujasiri—ninazungumza kama mtu asiye na akili—mimi pia ninatenda kwa ujasiri. 22 Je, wao ni Waebrania? Mimi pia.+ Je, wao ni Waisraeli? Mimi pia. Je, wao ni uzao wa* Abrahamu? Mimi pia.+ 23 Je, wao ni wahudumu wa Kristo? Ninajibu kama mwendawazimu, mimi ni mhudumu kwa njia kubwa hata zaidi: Nimefanya kazi nyingi zaidi,+ nimefungwa gerezani mara nyingi zaidi,+ nimepigwa mara nyingi sana, na kukaribia kufa mara nyingi.+ 24 Mara tano nilipigwa na Wayahudi viboko 40 kasoro kimoja,+ 25 mara tatu nilipigwa kwa fimbo,+ mara moja nilipigwa mawe,+ mara tatu nilivunjikiwa na meli,+ usiku mmoja na mchana mmoja nimekaa baharini; 26 mara nyingi katika safari, hatari za kutokana na mito, hatari za kutokana na wezi, hatari za kutokana na watu wangu mwenyewe,+ hatari za kutokana na mataifa,+ hatari jijini,+ hatari nyikani, hatari baharini, hatari kati ya ndugu wa uwongo, 27 kwa kazi ngumu na yenye kutaabisha, mara nyingi kukosa usingizi usiku,+ njaa na kiu,+ kukosa chakula mara nyingi,+ na pia baridi na kukosa mavazi.*
28 Zaidi ya mambo hayo ya nje, pia kuna jambo linalonipata siku kwa siku:* kuhangaikia makutaniko yote.+ 29 Ni nani aliye dhaifu, nami si dhaifu? Ni nani amekwazika, nami sina hasira?
30 Ikiwa ni lazima nijisifu, nitajisifu kuhusu mambo yanayoonyesha udhaifu wangu. 31 Mungu na Baba ya Bwana Yesu, Yule anayestahili kusifiwa milele, anajua sisemi uwongo. 32 Huko Damasko gavana aliye chini ya Areta mfalme alikuwa akilinda jiji la Wadamasko ili kunikamata, 33 lakini nilishushwa katika kapu kupitia dirisha kwenye ukuta wa jiji,+ nami nikaiponyoka mikono yake.
12 Lazima nijisifu. Hakuna faida, lakini nitaenda kwenye maono+ ya miujiza na ufunuo wa Bwana.+ 2 Ninamjua mtu fulani katika muungano na Kristo, ambaye miaka 14 iliyopita—kama ni katika mwili au nje ya mwili, sijui; Mungu anajua—alinyakuliwa mpaka kwenye mbingu ya tatu. 3 Ndiyo, ninamjua mtu kama huyo—iwe ni katika mwili au bila mwili, mimi sijui; Mungu anajua— 4 ambaye alinyakuliwa kuingia katika paradiso na kusikia maneno yasiyoweza kutamkwa na ambayo si halali kwa mtu kuyasema. 5 Nitajisifu kuhusu mtu wa namna hiyo, lakini sitajisifu kuhusu mimi mwenyewe isipokuwa kuhusu udhaifu wangu. 6 Kwa maana hata nikitaka kujisifu, sitakuwa mtu asiye na akili, kwa kuwa nitasema ukweli. Lakini sitaki kufanya hivyo, ili yeyote asinisifu zaidi ya yale anayoona kwangu au kusikia kutoka kwangu, 7 kwa sababu tu ya kupokea maono hayo ya ajabu.
Ili nisijiinue mno, nilipewa mwiba katika mwili,+ malaika wa Shetani, aendelee kunipiga kofi,* ili nisijiinue kupita kiasi. 8 Mara tatu nilimwomba Bwana kuhusu jambo hili, kwamba aniondolee. 9 Lakini akaniambia: “Fadhili zangu zisizostahiliwa zinakutosha, kwa kuwa nguvu zangu zinakamilika katika udhaifu.”+ Kwa furaha zaidi, basi, nitajisifu kuhusu udhaifu wangu, ili nguvu za Kristo zibaki juu yangu kama hema. 10 Basi ninapendezwa na udhaifu, na matusi, na nyakati za uhitaji, na mateso na shida, kwa ajili ya Kristo. Kwa maana ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa na nguvu.+
11 Nimekuwa mtu asiye na akili. Mlinilazimisha kuwa hivyo, kwa sababu ninyi mlipaswa kunipendekeza. Kwa maana hata katika jambo moja sikuwa mdogo kuliko mitume wenu walio bora sana, hata kama mimi si kitu.+ 12 Kwa kweli, ishara za mtume zilitokezwa kati yenu kwa uvumilivu mkubwa,+ na kwa ishara na mambo ya ajabu* na matendo yenye nguvu.+ 13 Ni kwa njia gani mlikosa kupendelewa kuliko makutaniko mengine, isipokuwa kwamba mimi mwenyewe sikuwa mzigo kwenu?+ Mnisamehe kosa hili kwa fadhili.
14 Tazama! Hii ni mara ya tatu niliyo tayari kuja kwenu, nami sitakuwa mzigo. Kwa kuwa ninawatafuta ninyi, si mali zenu;+ kwa maana watoto+ hawatarajiwi kuweka akiba kwa ajili ya wazazi wao, bali wazazi kwa ajili ya watoto wao. 15 Kwa upande wangu, nitatumia kwa furaha zaidi na kutumiwa kabisa kwa ajili yenu.*+ Kama nikiwapenda ninyi sana, je, mimi nipendwe kidogo? 16 Lakini hata iweje, mimi sikuwa mzigo kwenu.+ Hata hivyo mnasema, nilikuwa “mjanja” na niliwashika “kwa ujanja.” 17 Sikujifaidi kutoka kwenu kupitia yeyote kati ya wale niliowatuma kwenu, sivyo? 18 Nilimhimiza Tito na nikamtuma yule ndugu pamoja naye. Je, kweli Tito alijifaidi kutoka kwenu?+ Tulitembea katika roho ileile, sivyo? Katika hatua zilezile, sivyo?
19 Je, mnafikiri kwamba muda huu wote tumekuwa tukijitetea kwenu? Tunazungumza mbele za Mungu katika muungano na Kristo. Lakini wapendwa, yote tunayofanya ni kwa ajili ya kuwajenga. 20 Kwa maana ninaogopa kwamba huenda nitakapofika, sitawakuta mkiwa kama ninavyotaka nami sitakuwa kama mnavyotaka, badala yake, huenda kuna mizozo, wivu, milipuko ya hasira, migawanyiko, masengenyo, minong’ono,* kujivuna kwa kiburi, na machafuko. 21 Labda nitakapokuja tena, huenda Mungu wangu akaninyenyekeza mbele yenu, nami niwaombolezee wengi kati ya wale ambao mwanzoni walitenda dhambi lakini hawajatubu unajisi wao na uasherati* na mwenendo mpotovu* ambao wametenda.
13 Hii ni mara ya tatu ambayo ninakuja kwenu. “Kila jambo linapaswa kuthibitishwa kwa ushahidi wa* mashahidi wawili au watatu.”+ 2 Ingawa sipo sasa, ni kana kwamba nipo kwa mara ya pili, nami ninatoa onyo mapema kwa wale waliotenda dhambi mwanzoni na kwa wengine wote, kwamba ikiwa nitakuja tena sitawahurumia, 3 kwa kuwa mnatafuta uthibitisho kwamba Kristo, ambaye si dhaifu kuwaelekea ninyi bali ni mwenye nguvu kati yenu, kwa kweli anazungumza kupitia mimi. 4 Ni kweli kwamba aliuawa kwenye mti kwa sababu ya udhaifu, lakini yuko hai kwa sababu ya nguvu za Mungu.+ Ni kweli kwamba sisi pia ni dhaifu pamoja naye, lakini tutaishi pamoja naye+ kwa sababu ya nguvu za Mungu kuwaelekea ninyi.+
5 Endeleeni kujijaribu kama mko katika imani, endeleeni kuthibitisha jinsi ninyi wenyewe mlivyo.+ Au je, hamtambui kwamba Yesu Kristo yumo katika muungano pamoja nanyi? Isipokuwa muwe mmekataliwa. 6 Kwa kweli ninatumaini mtatambua kwamba hatujakataliwa.
7 Basi tunasali kwa Mungu kwamba msifanye kosa, si ili sisi tuonekane kuwa waliokubaliwa, bali mfanye yaliyo mema, hata tukionekana kwamba tumekataliwa. 8 Kwa maana hatuwezi kufanya jambo lolote kinyume cha kweli, bali kwa ajili ya kweli. 9 Hakika sisi hushangilia kila mara tunapokuwa dhaifu lakini ninyi mna nguvu. Nasi tunasali kwamba mrekebishwe upya. 10 Hiyo ndiyo sababu ninaandika mambo haya nikiwa sipo, ili nitakapokuja, nisiwe mkali katika kutumia mamlaka ambayo Bwana alinipa,+ ili kujenga na si kubomoa.
11 Mwishowe, akina ndugu, endeleeni kushangilia, kurekebishwa upya, kufarijiwa,+ kufikiri kwa upatano,+ kuishi kwa amani;+ na Mungu wa upendo na amani+ atakuwa pamoja nanyi. 12 Salimianeni kwa busu takatifu. 13 Watakatifu wote wanawatumia salamu zao.
14 Fadhili zisizostahiliwa za Bwana Yesu Kristo na upendo wa Mungu na ushirika katika roho takatifu ziwe pamoja nanyi nyote.
Au “hututia moyo.”
Au “dhiki.”
Au “dhiki.”
Au “dhiki.”
Au “kwa sababu ya nyuso nyingi zinazosali.”
Au labda, “yale ambayo tayari mnayajua vizuri.”
Tnn., “mpaka mwisho.”
Au labda, “ili mnufaike mara mbili.”
Pia anaitwa Sila.
Au “malipo ya awali; uthibitisho (dhamana) wa kile kitakachokuja.”
Au “dhidi ya nafsi yangu.”
Au “asimezwe.”
Au “asitudanganye.”
Au “nia; njama.”
Au “huitambulisha.”
Au “hatufanyi biashara; hatupati faida kutokana na.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Tnn., “kutoka utukufu mpaka utukufu.”
Angalia Nyongeza A5.
Au labda, “kupitia roho ya Yehova.”
Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Au “mwangaza wa.”
Au “katika mitungi ya udongo.”
Au labda, “tukiwa tumekata tamaa.”
Au “majaribu.”
Tnn., “ulio na uzito.”
Au “likivunjwa.”
Au “makao haya.”
Au “kuvaa makao yetu.”
Au “makao yetu ya mbinguni.”
Au “malipo ya awali; uthibitisho (dhamana) wa kile kitakachokuja.”
Au “tufunuliwe.”
Au “maovu.”
Au “tumefunuliwa.”
Au “tumefunuliwa.”
Au “dhabihu ya dhambi.”
Labda kwa ajili ya kushambulia.
Labda kwa ajili ya kujilinda.
Au “tunaonwa kama wanaostahili kifo.”
Au “waliotiwa nidhamu.”
Au “Tumezungumza waziwazi.”
Au “Hatujakosa nafasi ya.”
Au “ninyi pia panukeni.”
Au “Msiunganishwe.”
Kutokana na neno la Kiebrania linalomaanisha “Asiyefaa Kitu.” Linamrejelea Shetani.
Au “mtu mwaminifu.”
Au “mwamini ana fungu gani.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Tnn., “bidii yenu kwa ajili yangu.”
Au “kutamani sana kutubu.”
Au “safi kiadili; bila hatia.”
Au labda, “nitakuwa na ujasiri mwingi kwa sababu yenu.”
Au “ufurike.”
Angalia Nyongeza A5.
Tnn., “mshiriki.”
Au “bila kutaka.”
Au “kwa ukarimu.”
Tnn., “jinsi tulivyo katika maneno.”
Tnn., “tutakuwa hivyo pia katika matendo.”
Au “alitugawia kwa kipimo.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Tnn., “bidii ya Mungu.”
Au “safi kiadili.”
Au “usafi wa kiadili.”
Au “Niliyapora.”
Au “msaada.”
Au “kisingizio cha.”
Au “cheo ambacho.”
Yaani, kwa maoni ya wanadamu.
Tnn., “mbegu ya.”
Tnn., “katika uchi.”
Au “kuna mambo yanayonikaza kila siku kuhusu.”
Au “kunipiga.”
Au “miujiza.”
Au “nafsi zenu.”
Au “umbeya.”
Neno la Kigiriki, por·neiʹa. Angalia Kamusi.
Au “ufidhuli; matendo ya kuchukiza yanayofanywa bila aibu.” Kigiriki, a·selʹgei·a. Angalia Kamusi.
Tnn., “kinywa cha.”