Kwa Waefeso
1 Paulo, mtume+ wa Kristo Yesu kupitia mapenzi ya Mungu,+ kwa watakatifu walio katika Efeso na waaminifu+ katika muungano+ na Kristo Yesu:
2 Na muwe na fadhili zisizostahiliwa+ na amani+ kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo.
3 Abarikiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo,+ kwa kuwa ametubariki+ kwa kila aina ya baraka ya kiroho katika mahali pa kimbingu+ katika muungano na Kristo, 4 kama vile alivyotuchagua+ katika muungano naye kabla ya kuwekwa msingi+ wa ulimwengu, ili tuwe watakatifu na bila dosari+ mbele zake katika upendo.+ 5 Kwa maana alituagiza kimbele+ ili tufanywe kuwa wana+ kwake kupitia Yesu Kristo,+ kulingana na upendezi mwema wa mapenzi yake,+ 6 kwa sifa+ ya fadhili zake zisizostahiliwa+ zenye utukufu alizotupatia kwa fadhili kwa njia ya mpendwa wake.+ 7 Kwa njia yake tuna kuachiliwa huru kwa njia ya fidia kupitia damu+ ya huyo, ndiyo, msamaha+ wa makosa yetu, kulingana na utajiri wa fadhili zake zisizostahiliwa.+
8 Alituzidishia hizo katika hekima+ yote na akili nzuri, 9 kwa kuwa alitujulisha siri takatifu+ ya mapenzi yake. Ni kulingana na upendezi wake mwema alioukusudia ndani yake mwenyewe+ 10 kwa ajili ya usimamizi+ wa mambo kwenye kikomo kamili cha nyakati+ zilizowekwa rasmi, yaani, kukusanya tena pamoja+ vitu vyote katika Kristo,+ vitu vilivyo mbinguni+ na vitu vilivyo duniani.+ Ndiyo, katika yeye, 11 katika muungano pamoja na yeye ambaye tulihesabiwa pia kuwa warithi,+ kwa kuwa tuliagizwa kimbele kulingana na kusudi lake yeye anayetenda mambo yote kulingana na jinsi mapenzi yake yanavyoshauri,+ 12 ili tupate kuwa kwa ajili ya sifa ya utukufu wake,+ sisi ambao tumekuwa wa kwanza kumtumaini Kristo.+ 13 Lakini ninyi pia mlimtumaini yeye baada ya kulisikia neno la kweli,+ habari njema juu ya wokovu+ wenu. Kupitia yeye pia, baada ya ninyi kuamini, mlitiwa muhuri+ kwa roho takatifu iliyoahidiwa,+ 14 ambayo ni rehani+ ya kimbele ya urithi+ wetu, kwa kusudi la kuiachilia huru kupitia fidia+ mali+ ya Mungu mwenyewe, kwa sifa yake yenye utukufu.
15 Hiyo ndiyo sababu mimi pia, kwa kuwa nimesikia juu ya imani mliyo nayo katika Bwana Yesu na kuwaelekea watakatifu wote,+ 16 siachi kutoa shukrani kwa ajili yenu. Naendelea kuwataja ninyi katika sala zangu,+ 17 ili Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa utukufu, awape ninyi roho ya hekima+ na ya ufunuo katika ujuzi sahihi juu yake;+ 18 macho+ ya moyo wenu yakiwa yametiwa nuru,+ ili mjue jinsi lilivyo lile tumaini+ alilowaitia, jinsi ulivyo utajiri wenye utukufu+ ambao amewawekea watakatifu kuwa urithi,+ 19 na jinsi zilivyo kuu zaidi nguvu+ zake kutuelekea sisi tulio waamini. Ni kulingana na utendaji+ wa uwezo wa nguvu zake, 20 ambao kwa huo ametenda kuhusiana na Kristo alipomfufua kutoka kwa wafu+ na kumketisha kwenye mkono wake wa kuume+ katika mahali pa kimbingu,+ 21 juu zaidi kuliko kila serikali na mamlaka na nguvu na utawala+ na kila jina linalotajwa,+ si katika mfumo huu wa mambo+ tu, bali pia katika ule ujao.+ 22 Alivitiisha pia vitu vyote chini ya miguu yake,+ na kumfanya kuwa kichwa juu ya vitu vyote+ kuhusiana na kutaniko, 23 ambalo ni mwili wake,+ ujazo+ wake anayejaza vitu vyote katika vyote.+
2 Zaidi ya hilo, ninyi ndio ambao Mungu alifanya kuwa hai ingawa mlikuwa wafu katika makosa na dhambi zenu,+ 2 ambazo wakati fulani mlitembea ndani yake kulingana na mfumo wa mambo+ wa ulimwengu huu, kulingana na mtawala+ wa mamlaka ya hewa, roho+ ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii.+ 3 Ndiyo, wakati fulani sisi sote tulijiendesha katikati yao kupatana na tamaa za mwili wetu,+ tukifanya mambo yanayopendwa na mwili+ na fikira, nasi kiasili tulikuwa watoto wa ghadhabu+ sawa na wale wengine. 4 Lakini Mungu, aliye tajiri katika rehema,+ kwa upendo wake mkubwa aliotupenda nao,+ 5 alitufanya hai pamoja na Kristo, tulipokuwa wafu katika makosa+—kwa fadhili zisizostahiliwa ninyi mmeokolewa+— 6 naye alituinua+ pamoja na kutuketisha pamoja katika mahali pa kimbingu+ katika muungano na Kristo Yesu, 7 ili katika mifumo ya mambo inayokuja+ uonyeshwe utajiri+ mwingi zaidi wa fadhili zake zisizostahiliwa katika neema yake kutuelekea sisi katika muungano+ na Kristo Yesu.
8 Kwa fadhili hizi zisizostahiliwa, kwa kweli, ninyi mmeokolewa kupitia imani;+ na hiyo si kutokana na ninyi,+ ni zawadi ya Mungu.+ 9 Hapana, si kutokana na matendo,+ ili mtu yeyote asiwe na sababu ya kujisifu.+ 10 Kwa maana sisi ni matokeo ya kazi yake+ na tuliumbwa+ katika muungano+ na Kristo Yesu kwa ajili ya matendo mema,+ ambayo Mungu alitutayarishia kimbele+ ili tutembee katika hayo.
11 Kwa hiyo endeleeni kukumbuka akilini kwamba hapo zamani mlikuwa watu wa mataifa kwa habari ya mwili;+ “kutotahiriwa” ndivyo mlivyoitwa na kile kinachoitwa “kutahiriwa” ambacho kimefanywa mwilini kwa mikono+— 12 kwamba wakati huo mlikuwa bila Kristo,+ mlikuwa mmetengwa mbali+ na taifa la Israeli nanyi mlikuwa wageni kwa maagano ya ahadi,+ wala hamkuwa na tumaini+ na mlikuwa bila Mungu katika ulimwengu.+ 13 Lakini sasa katika muungano na Kristo Yesu ninyi ambao wakati mmoja mlikuwa mbali sana mmekuja kuwa karibu kupitia damu+ ya Kristo. 14 Kwa maana yeye ni amani yetu,+ yeye aliyefanya vile vikundi viwili+ kuwa kimoja+ na kuuharibu ukuta+ wa katikati uliowatenganisha.+ 15 Kwa njia ya mwili wake+ aliufuta uadui,+ ile Sheria ya amri zilizofanyizwa kwa maagizo,+ ili aumbe vile vikundi viwili vya watu+ katika muungano na yeye mwenyewe viwe mtu mmoja mpya+ na kufanya amani; 16 na ili avipatanishe+ kwa ukamili hivyo vikundi viwili vya watu+ katika mwili mmoja kwa Mungu kupitia mti wa mateso,+ kwa sababu alikuwa ameua ule uadui+ kwa njia ya yeye mwenyewe. 17 Naye alikuja na kuwatangazia ninyi habari njema ya amani,+ wale waliokuwa mbali sana, na amani kwa wale waliokuwa karibu,+ 18 kwa sababu kupitia yeye, sisi, vikundi vyote viwili vya watu,+ tunaweza kumkaribia+ Baba kwa roho moja.+
19 Hakika, basi, ninyi si wageni+ tena na wakaaji wageni,+ bali ninyi ni raia wenzi+ wa watakatifu+ na ni washiriki wa nyumba+ ya Mungu, 20 nanyi mmejengwa juu ya msingi+ wa mitume+ na manabii,+ naye Kristo Yesu mwenyewe akiwa ndiye jiwe la msingi la pembeni.+ 21 Katika muungano na yeye, jengo lote likiunganishwa pamoja+ kwa upatano, linakua liwe hekalu takatifu kwa ajili ya Yehova.+ 22 Katika muungano+ na yeye, ninyi pia mnajengwa pamoja muwe mahali pa Mungu pa kukaa kwa njia ya roho.+
3 Kwa hiyo mimi, Paulo, mfungwa+ wa Kristo Yesu kwa ajili yenu, watu wa mataifa+— 2 ikiwa, kwa kweli, mmesikia juu ya usimamizi-nyumba+ wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu ambao nilipewa kwa ajili yenu, 3 kwamba nilijulishwa siri takatifu kwa njia ya ufunuo,+ kama vile nilivyoandika kwa ufupi hapo mwanzoni. 4 Kwa kufikiria haya, mnapoisoma hii, mnaweza kuona utambuzi+ nilio nao katika siri takatifu+ ya Kristo. 5 Katika vizazi vingine siri hii+ haikujulishwa kwa wana wa binadamu kama vile ambavyo imefunuliwa+ sasa kwa mitume wake watakatifu na manabii+ kupitia roho, 6 yaani, kwamba watu wa mataifa wawe warithi wa pamoja na viungo vyenzi vya mwili+ na washiriki pamoja nasi wa ahadi+ katika muungano na Kristo Yesu kupitia habari njema. 7 Mimi nilikuja kuwa mhudumu+ wa hilo kulingana na zawadi ya bure ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu nilizopewa kulingana na njia ambayo nguvu zake hutenda.+
8 Mimi, niliye mtu mdogo kuliko aliye mdogo+ zaidi kati ya watakatifu wote, nilipewa fadhili hizi zisizostahiliwa,+ ili niwatangazie mataifa+ habari njema juu ya utajiri+ usiopimika wa Kristo 9 na kufanya watu waone jinsi siri takatifu+ inavyosimamiwa+ ambayo tangu wakati uliopita usio na kipimo imefichwa katika Mungu, aliyeviumba vitu vyote.+ 10 Hiyo ilikuwa kwa kusudi kwamba sasa serikali na mamlaka+ zilizo katika mahali pa kimbingu zijulishwe kupitia kutaniko+ hekima ya Mungu ya namna nyingi sana,+ 11 kulingana na kusudi la milele alilofanyiza kuhusiana na Kristo,+ Yesu Bwana wetu, 12 ambaye kwa njia yake tuna uhuru huu wa kusema na tuna uwezo wa kukaribia+ tukiwa na uhakika kupitia imani yetu katika yeye. 13 Kwa hiyo nawaomba ninyi msife moyo kwa sababu ya hizi dhiki+ zangu kwa ajili yenu, kwa maana hizi zinamaanisha utukufu kwenu.
14 Kwa sababu hiyo nampigia Baba magoti,+ 15 ambaye kila familia+ mbinguni na duniani hupata jina kutokana naye,+ 16 kwa kusudi la kwamba awawezeshe ninyi kulingana na utajiri+ wa utukufu wake mfanywe kuwa na uwezo katika mtu mliye kwa ndani+ mkiwa na nguvu kupitia roho yake,+ 17 ili muwe na Kristo akikaa kupitia imani yenu katika mioyo yenu kwa upendo;+ ili mtie mizizi+ na kuimarishwa juu ya ule msingi,+ 18 ili mweze kufahamu kabisa akilini+ pamoja na watakatifu wote, upana na urefu na kimo na kina,+ 19 na kuujua upendo wa Kristo+ ambao unazidi ujuzi, ili mjawe na ujazo+ wote ambao Mungu hutoa.
20 Basi kwa yeye anayeweza, kulingana na nguvu zake zinazotenda+ ndani yetu, kufanya kwa wingi zaidi kupita mambo yote tunayoomba au tunayofikiri,+ 21 kwake kuwe na utukufu kwa njia ya kutaniko na kwa njia ya Kristo Yesu kwa vizazi vyote milele na milele.+ Amina.
4 Kwa hiyo, mimi, niliye mfungwa+ katika Bwana, nawasihi ninyi mtembee kwa kuustahili+ mwito mlioitiwa,+ 2 mkiwa na unyenyekevu kamili wa akili+ na upole, mkiwa na ustahimilivu,+ mkivumiliana katika upendo,+ 3 mkijitahidi sana kuushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani.+ 4 Kuna mwili mmoja,+ na roho moja,+ kama vile mlivyoitwa katika tumaini+ moja mliloitiwa; 5 Bwana mmoja,+ imani moja,+ ubatizo mmoja;+ 6 Mungu mmoja+ na Baba wa watu wote, aliye juu ya wote na kupitia wote na katika wote.
7 Basi kila mmoja wetu alipewa fadhili zisizostahiliwa+ kulingana na jinsi Kristo alivyoipima hiyo zawadi ya bure.+ 8 Kwa hiyo anasema: “Alipopanda juu alichukua mateka; alitoa zawadi katika wanadamu.”+ 9 Basi neno “alipopanda,”+ linamaanisha nini isipokuwa kwamba alishuka pia katika maeneo ya chini zaidi, yaani, dunia?+ 10 Yule aliyeshuka ndiye pia aliyepanda+ juu zaidi ya mbingu+ zote, ili avijaze+ vitu vyote.
11 Naye alitoa wengine kuwa mitume,+ wengine kuwa manabii,+ wengine kuwa waeneza-injili,+ wengine kuwa wachungaji na walimu,+ 12 kwa kusudi la kuwarekebisha+ upya watakatifu, kwa ajili ya kazi ya huduma, kwa ajili ya kuujenga mwili wa Kristo,+ 13 mpaka sisi sote tuufikie umoja katika imani na katika ujuzi sahihi wa Mwana wa Mungu, kufikia kuwa mtu aliyekomaa,+ kufikia kipimo cha kimo ambacho ni cha ujazo wa Kristo;+ 14 ili tusiwe tena watoto wachanga, tukirushwa huku na huku+ kama kwa mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho+ kupitia udanganyifu+ wa watu, kwa njia ya ujanja katika kutunga kosa. 15 Lakini tukisema kweli,+ na tukue kwa upendo+ katika mambo yote ndani yake yeye aliye kichwa,+ Kristo. 16 Kutoka katika yeye mwili wote,+ kwa kuunganishwa pamoja kwa upatano na kufanywa ushirikiane kupitia kila kiungo ambacho hutoa kile kinachohitajiwa, kulingana na utendaji wa kila kiungo kimoja-kimoja katika kipimo kinachofaa, hutokeza ukuzi wa mwili ili huo ujijenge wenyewe katika upendo.+
17 Kwa hiyo, nasema hili na kulitolea ushahidi katika Bwana, kwamba msiendelee tena kutembea kama vile mataifa+ wanavyotembea pia katika ubatili wa akili+ zao, 18 huku wakiwa katika giza kiakili,+ na kutenganishwa mbali+ na uzima ambao ni wa Mungu, kwa sababu ya kule kutojua+ ambako kumo ndani yao, kwa sababu ya ugumu+ wa mioyo yao. 19 Wakiisha kuishiwa na ufahamu wote wa maadili,+ walijitoa wenyewe ili kuwa na mwenendo mpotovu+ na kufanya ukosefu wa usafi+ wa kila namna kwa pupa.+
20 Lakini ninyi hamkujifunza Kristo kuwa hivyo,+ 21 mradi tu mlimsikia yeye na mlifundishwa kupitia yeye,+ kama vile kweli+ ilivyo katika Yesu, 22 kwamba mnapaswa kuuondolea mbali utu wa zamani+ unaolingana na mwenendo wenu wa kwanza na ambao unaharibiwa+ kulingana na tamaa zake za udanganyifu;+ 23 bali kwamba mnapaswa kufanywa upya katika nguvu zinazoendesha akili yenu,+ 24 na mnapaswa kuvaa+ utu mpya+ ulioumbwa+ kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli+ na ushikamanifu.
25 Kwa hiyo, sasa kwa kuwa mmeuondolea mbali uwongo,+ semeni kweli kila mmoja wenu na jirani yake,+ kwa sababu sisi ni viungo vya mtu na mwenzake.+ 26 Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi;+ jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka,+ 27 wala msimpe Ibilisi nafasi.+ 28 Mwizi asiibe tena,+ bali afanye kazi ya bidii, akifanya kwa mikono yake kazi iliyo njema,+ ili awe na kitu cha kumgawia mtu aliye na uhitaji.+ 29 Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu,+ bali neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwape wasikiaji lile linalofaa.+ 30 Pia, msiwe mkiihuzunisha roho takatifu+ ya Mungu, ambayo kupitia hiyo mmetiwa muhuri+ kwa ajili ya siku ya kuachiliwa huru kupitia fidia.+
31 Uchungu wote wenye uovu+ na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano+ na viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.+ 32 Bali iweni wenye fadhili+ ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo,+ mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari.+
5 Kwa hiyo, iweni waigaji wa Mungu,+ kama watoto wapendwa, 2 na endeleeni kutembea katika upendo,+ kama vile Kristo pia alivyowapenda ninyi+ na kujitoa mwenyewe kwa ajili yenu kuwa toleo+ na dhabihu kwa Mungu ili kuwa harufu tamu.+
3 Uasherati+ na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa+ visitajwe hata kidogo katikati yenu,+ kama inavyowafaa watu watakatifu;+ 4 wala mwenendo wa aibu+ wala maneno ya kipumbavu wala mizaha michafu,+ mambo yasiyofaa, lakini badala ya hayo, utoaji wa shukrani.+ 5 Kwa maana mnajua hili, nanyi mnalitambua wenyewe, kwamba hakuna mwasherati+ au mtu asiye safi au mtu mwenye pupa+—maana yake ni kuwa mwabudu-sanamu—aliye na urithi wowote katika ufalme wa Kristo na wa Mungu.+
6 Mtu yeyote asiwadanganye ninyi kwa maneno matupu,+ kwa maana kwa sababu ya mambo yaliyotangulia kusemwa ghadhabu ya Mungu inakuja juu ya wana wa kutotii.+ 7 Kwa hiyo msishirikiane pamoja nao;+ 8 kwa maana wakati mmoja ninyi mlikuwa giza,+ bali sasa ninyi ni nuru+ kuhusiana na Bwana. Endeleeni kutembea kama watoto wa nuru, 9 kwa maana matunda ya nuru yana kila namna ya wema na uadilifu na kweli.+ 10 Endeleeni kuhakikisha lile linalokubalika+ kwa Bwana; 11 na mwache kushirikiana+ pamoja nao katika matendo yasiyozaa matunda, ambayo ni ya giza,+ lakini badala yake muwe hata mkiyakaripia,+ 12 kwa maana mambo ambayo wao hutenda katika siri hata kuyasimulia ni aibu.+ 13 Basi mambo yote yanayokaripiwa+ yanafunuliwa na nuru, kwa maana kila jambo linalofunuliwa+ ni nuru. 14 Kwa hiyo yeye anasema: “Amka,+ Ee mwenye kulala usingizi, na ufufuke kutoka kwa wafu,+ na Kristo atakuangaza.”+
15 Kwa hiyo endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea+ si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, 16 mkijinunulia wakati unaofaa,+ kwa sababu siku hizi ni zenye uovu.+ 17 Kwa hiyo mwache kuwa wenye kukosa akili, bali endeleeni kufahamu+ yale yaliyo mapenzi+ ya Yehova. 18 Pia, msiwe mkilewa+ divai, ambayo ina upotovu ndani yake,+ bali endeleeni kujazwa na roho,+ 19 mkijisemesha kwa zaburi+ na sifa+ kwa Mungu na nyimbo za kiroho, mkiimba+ na kupiga muziki+ katika mioyo yenu kwa Yehova, 20 katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo mkimtolea shukrani+ sikuzote Mungu na Baba yetu kwa ajili ya mambo yote.
21 Jitiisheni kwa mmoja na mwenzake+ katika kumwogopa Kristo. 22 Wake na wajitiishe+ kwa waume zao kama kwa Bwana, 23 kwa sababu mume ni kichwa cha mke+ wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko,+ yeye akiwa mwokozi wa mwili huu. 24 Kwa kweli, kama kutaniko linavyojitiisha kwa Kristo, vivyo hivyo wanawake pia na wajitiishe kwa waume zao katika mambo yote.+ 25 Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu,+ kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake,+ 26 ili alitakase,+ akilisafisha na kuliosha kwa maji kwa njia ya neno,+ 27 ili kujipa mwenyewe kutaniko likiwa na fahari,+ likiwa bila doa au kunyanzi au lolote la mambo hayo, bali ili liwe takatifu na bila dosari.+
28 Vivyo hivyo waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Yeye anayempenda mke wake anajipenda mwenyewe, 29 kwa maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake kwa vyovyote; bali huulisha na kuutunza+ kwa upendo, kama vile Kristo pia anavyolitendea kutaniko, 30 kwa sababu sisi ni viungo vya mwili wake.+ 31 “Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja.”+ 32 Siri hii takatifu+ ni kubwa. Sasa ninasema kwa habari ya Kristo na kutaniko.+ 33 Hata hivyo, pia, kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake+ kama vile anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu+ sana mume wake.
6 Enyi watoto, watiini wazazi+ wenu katika muungano+ na Bwana, kwa maana hilo ni jambo la uadilifu:+ 2 “Mheshimu baba yako na mama yako”;+ ambayo ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi:+ 3 “Ili mambo yakuendee vema nawe ukae muda mrefu duniani.”+ 4 Nanyi, akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu,+ bali endeleeni kuwalea+ katika nidhamu+ na mwongozo wa akilini+ wa Yehova.
5 Enyi watumwa, watiini wale ambao ni mabwana wenu katika maana ya kimwili,+ kwa kuogopa na kutetemeka+ katika unyoofu wa mioyo yenu, kama vile kwa Kristo, 6 si kwa njia ya utumishi wa macho kama wanavyofanya wale wanaowapendeza wanadamu,+ bali kama watumwa wa Kristo, mkiyafanya mapenzi ya Mungu kwa nafsi yote.+ 7 Iweni watumwa mkiwa na maelekeo mema, kama kwa Yehova,+ wala si kwa wanadamu, 8 kwa maana mnajua kwamba wema wowote ambao huenda kila mmoja akafanya, Yehova atamlipa+ huo, hata kama yeye ni mtumwa au ni mtu huru.+ 9 Pia, enyi mabwana, endeleeni kuwatendea wao mambo hayohayo, na mwache kutisha,+ kwa maana mnajua kwamba Bwana wao na wenu+ pia yuko mbinguni, naye hana ubaguzi+ wowote.
10 Mwishowe, endeleeni kujipatia nguvu+ katika Bwana na katika uwezo+ wa nguvu zake. 11 Vaeni mavazi kamili ya silaha+ kutoka kwa Mungu ili mweze kusimama imara kupinga hila+ za Ibilisi; 12 kwa sababu tuna kushindana mweleka,+ si juu ya damu na mwili, bali juu ya serikali,+ juu ya mamlaka,+ juu ya watawala wa ulimwengu+ wa giza hili, juu ya majeshi ya roho waovu+ katika mahali pa kimbingu. 13 Kwa sababu hiyo chukueni mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu,+ ili mweze kupinga katika ile siku ya uovu, baada ya ninyi kufanya mambo yote kwa ukamili, mweze kusimama imara.+
14 Kwa hiyo, simameni imara, viuno vyenu+ vikiwa vimefungwa kwa ile kweli,+ na mkiwa mmevaa bamba la kifuani la uadilifu,+ 15 na mkiwa mmevaa miguuni+ mwenu viatu vya habari njema ya amani.+ 16 Zaidi ya mambo yote, ichukueni ngao kubwa ya imani,+ ambayo kwa kuitumia mtaweza kuizima mishale yote inayowaka moto ya yule mwovu.+ 17 Pia, ipokeeni kofia ya chuma+ ya wokovu, na upanga+ wa roho,+ yaani, neno la Mungu,+ 18 huku kwa kila namna ya sala+ na dua mkiendeleza sala kila wakati katika roho.+ Na kwa kusudi hilo endeleeni kukaa macho daima na kuomba dua kwa ajili ya watakatifu wote, 19 pia kwa ajili yangu, ili nipewe uwezo wa kusema+ kwa kufungua kinywa changu, kwa uhuru wa kusema+ ili kujulisha siri takatifu ya habari njema,+ 20 ambayo kwa ajili yake ninatenda kama balozi+ aliyefungwa minyororo; ili niweze kusema kuhusiana nayo kwa ujasiri kama ninavyopaswa kusema.+
21 Basi ili ninyi mjue pia juu ya mambo yangu, kuhusu jinsi ninavyoendelea, Tikiko,+ ndugu mpendwa na mhudumu mwaminifu katika Bwana, atawajulisha ninyi kila jambo.+ 22 Ninamtuma kwenu kwa kusudi hilo, ili myajue mambo yetu na ili aifariji mioyo yenu.+
23 Akina ndugu na wawe na amani na upendo pamoja na imani kutoka kwa Mungu Baba na Bwana Yesu Kristo. 24 Fadhili zisizostahiliwa+ na ziwe pamoja na wale wote wanaompenda Bwana wetu Yesu Kristo katika hali ya kutokuharibika.