Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • bi12 Ruthu 1:1-4:22
  • Ruthu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ruthu
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Ruthu

Ruthu

1 Basi ikawa katika siku ambazo waamuzi+ walitekeleza haki, njaa+ ikatokea nchini, na mwanamume mmoja akatoka Bethlehemu+ katika Yuda, akakae akiwa mgeni katika nchi ya Moabu,+ yeye na mke wake na wanawe wawili. 2 Mwanamume huyo aliitwa Elimeleki, na mke wake aliitwa Naomi, nao wanawe wawili waliitwa Maloni na Kilioni, Waefrathi+ kutoka Bethlehemu katika Yuda. Mwishowe wakafika katika nyanda za Moabu, wakakaa huko.

3 Baada ya muda Elimeleki mume wa Naomi akafa, naye akabaki na wanawe wawili. 4 Baadaye wanaume hao wakajichukulia wake, wanawake Wamoabu.+ Mmoja aliitwa Orpa, na yule mwingine Ruthu.+ Wakakaa huko yapata miaka kumi. 5 Baada ya muda, wote wawili, Maloni na Kilioni, wakafa pia, naye mwanamke huyo akabaki bila watoto wake wawili wala mume wake. 6 Naye akaondoka na binti-wakwe zake, na kurudi kutoka katika nyanda za Moabu, kwa maana alikuwa amesikia katika uwanda wa Moabu kwamba Yehova alikuwa ameelekeza fikira zake kwa watu wake+ na kuwapa mkate.+

7 Naye akaondoka hapo alipokuwa amekaa,+ nao binti-wakwe zake wawili walikuwa pamoja naye. Wakatembea barabarani kurudi nchi ya Yuda. 8 Mwishowe Naomi akawaambia: “Nendeni, rudini, kila mmoja nyumbani kwa mama yake. Yehova na awaonyeshe fadhili zenye upendo,+ kama vile tu mlivyowaonyesha wanaume hawa ambao sasa wamekufa na mimi pia.+ 9 Yehova na awape zawadi,+ na mpate mahali pa kupumzika+ kila mmoja katika nyumba ya mume wake.” Kisha akawabusu,+ nao wakaanza kupaaza sauti zao na kulia. 10 Nao wakawa wakimwambia: “Hapana, bali tutarudi pamoja nawe kwa watu wako.”+ 11 Lakini Naomi akasema: “Rudini, binti zangu. Kwa nini mwende na mimi? Je, bado nina wana ndani yangu, na je, watakuwa waume zenu?+ 12 Rudini, binti zangu, nendeni, kwa maana mimi nimezeeka sana nisiweze kupata mume. Ikiwa ningesema kwamba nilikuwa na tumaini pia kwamba hakika nitapata mume usiku wa leo na pia nipate kuzaa wana,+ 13 je, mngewangojea mpaka wawe wakubwa? Je, mngejitenga kwa ajili yao hivi kwamba msipate kuwa wake za waume wengine? Hapana, binti zangu, kwa maana nina uchungu sana kwa sababu yenu, kwamba mkono wa Yehova umenigeukia.”+

14 Basi wakapaaza sauti zao na kulia tena, halafu Orpa akambusu mama-mkwe wake. Bali Ruthu akashikamana naye.+ 15 Kwa hiyo akasema: “Tazama! Shemeji yako amerudi kwa watu wake na kwa miungu yake.+ Rudi pamoja naye.”+

16 Naye Ruthu akasema: “Usiniombe nikuache, nigeuke nisifuatane nawe; kwa maana uendako nitaenda, na mahali utakapokaa usiku kucha nitakaa.+ Watu wako watakuwa watu wangu,+ na Mungu wako Mungu wangu.+ 17 Pale utakapokufa nitakufa nami,+ na hapo ndipo nitakapozikwa. Yehova na anitende hivyo na kuzidi+ ikiwa chochote isipokuwa kifo kitatutenganisha mimi na wewe.”

18 Alipoona kwamba anasisitiza kwenda naye,+ akaacha kusema naye. 19 Nao wote wawili wakaenda mpaka walipofika Bethlehemu.+ Ikawa mara tu walipofika Bethlehemu, habari zao zikavuma kote jijini,+ nao wanawake wakauliza-uliza: “Je, huyu ni Naomi?”+ 20 Naye akawa akiwajibu: “Msiniite Naomi. Niiteni Mara, kwa maana Mweza-Yote+ amenifanya kuwa na uchungu sana.+ 21 Nilikuwa nimejaa nilipoenda,+ naye Yehova amenifanya nirudi mikono mitupu.+ Kwa nini mniite Naomi, hali Yehova ndiye amenifedhehesha+ na Mweza-Yote ndiye amenisababishia msiba?”+

22 Hivyo ndivyo alivyorudi Naomi pamoja na Ruthu Mmoabu, binti-mkwe wake, walipokuwa wakirudi kutoka katika nyanda za Moabu;+ nao wakafika Bethlehemu+ mwanzoni mwa mavuno ya shayiri.+

2 Basi Naomi alikuwa na mtu wa ukoo+ wa mume wake, mwenye mali nyingi,+ wa familia ya Elimeleki, aliyeitwa Boazi.+

2 Baada ya muda Ruthu yule mwanamke Mmoabu akamwambia Naomi: “Tafadhali, acha niende shambani nikaokote masalio+ katikati ya masuke ya nafaka nyuma ya yeyote yule nitakayepata kibali machoni pake.” Basi akamwambia: “Nenda, binti yangu.” 3 Basi akatoka, akaenda, akaingia na kuanza kuokota masalio katika shamba nyuma ya wavunaji.+ Ikatukia kwamba alikuwa katika shamba la Boazi,+ aliyekuwa wa familia ya Elimeleki.+ 4 Na, tazama! Boazi akaja kutoka Bethlehemu na kuwaambia wavunaji: “Yehova na awe pamoja nanyi.”+ Nao wakamjibu: “Yehova na akubariki wewe.”+

5 Kisha Boazi+ akamuuliza kijana aliyewekwa juu ya wavunaji: “Huyu mwanamke kijana ni wa nani?” 6 Basi kijana huyo akamjibu na kusema: “Ni Mmoabu,+ aliyerudi na Naomi kutoka katika uwanda wa Moabu.+ 7 Naye alisema, ‘Tafadhali niruhusu niokote masalio,+ nami nitaokota katikati ya masuke yaliyokatwa ya nafaka nyuma ya wavunaji.’ Basi akaingia naye hajaketi tangu wakati huo asubuhi mpaka sasa hivi alipoketi ndani ya nyumba kwa kitambo kidogo.”+

8 Baadaye Boazi akamwambia Ruthu: “Umesikia binti yangu, sivyo? Usiende kuokota masalio katika shamba lingine,+ wala usivuke kutoka hapa, kwa hiyo ukae karibu na wanawake wangu vijana.+ 9 Macho yako na yawe katika shamba watakalovuna, nawe uende nao. Je, sikuwaamuru vijana wasikuguse?+ Unapokuwa na kiu, uende kwenye vyombo, ukanywe waliyoyateka+ hao vijana.”

10 Kisha akaanguka kifudifudi, akainama,+ akamwambia: “Nimewezaje kupata kibali machoni pako hivi kwamba natambuliwa, hali mimi ni mgeni?”+ 11 Ndipo Boazi akajibu na kumwambia: “Nilipewa habari+ kamili juu ya yote ambayo umemfanyia mama-mkwe wako baada ya kifo cha mume wako.+ Pia jinsi ulivyowaacha baba yako na mama yako na nchi ya watu wa jamaa yako na kwenda kwa kikundi cha watu ambao hukuwa umewajua zamani.+ 12 Yehova na akupe thawabu kwa sababu ya jinsi unavyotenda,+ na upate malipo kamili+ kutoka kwa Yehova Mungu wa Israeli, ambaye umekuja kutafuta kimbilio chini ya mabawa yake.”+ 13 Basi akasema: “Acha nipate kibali machoni pako, bwana wangu, kwa sababu umenifariji na kwa sababu umesema kwa kumtuliza mjakazi wako,+ ingawa mimi mwenyewe huenda nisiwe kama mmoja wa wajakazi wako.”+

14 Boazi akamwambia walipokuwa wakila: “Karibia hapa, ule baadhi ya mikate+ na kuchovya kipande chako katika siki.” Basi akaketi kando ya wavunaji. Boazi alikuwa akimpatia nafaka zilizochomwa+ ale. Akala, akatosheka, na tena akabakiza. 15 Kisha akasimama aokote masalio.+ Basi Boazi akawaamuru wanaume wake vijana, akisema: “Mwacheni aokote masalio katikati ya masuke ya nafaka yaliyokatwa pia, nanyi msimsumbue.+ 16 Pia mhakikishe mmemtolea baadhi yake katika vitita vya masuke, na kuyaacha nyuma apate kuyaokota,+ wala msimkemee.”

17 Basi akaokota masalio shambani mpaka jioni.+ Akapura+ masalio aliyokuwa ameokota. Yakawa karibu efa+ moja ya shayiri. 18 Halafu akayachukua na kwenda jijini. Mama-mkwe wake akaona masalio aliyokuwa ameokota. Naye Ruthu akatoa chakula alichokuwa amebakiza+ alipokuwa ameshiba, akampa.

19 Basi mama-mkwe wake akamuuliza: “Uliokota masalio wapi leo, nawe ulifanya kazi wapi? Yule aliyekuona na abarikiwe.”+ Ndipo akamwambia alikuwa amefanya kazi na nani; naye akasema: “Jina la mwanamume niliyefanya kazi naye leo ni Boazi.” 20 Kisha Naomi akamwambia: “Na abarikiwe huyo na Yehova,+ ambaye hakuacha kuonyesha fadhili zake zenye upendo+ kwa walio hai na wafu.”+ Naye Naomi akamwambia: “Mwanamume huyo ni wa jamaa yetu.+ Yeye ni mmoja wa wakombozi wetu.”+ 21 Halafu Ruthu Mmoabu akasema: “Pia aliniambia, ‘Ukae karibu na vijana wangu mpaka watakapomaliza mavuno yote niliyo nayo.’”+ 22 Basi Naomi+ akamwambia Ruthu binti-mkwe wake:+ “Binti yangu, ni afadhali uende na wanawake wake vijana, usije ukasumbuliwa katika shamba lingine.”+

23 Naye akaendelea kukaa karibu na wanawake vijana wa Boazi na kuokota masalio mpaka mavuno ya shayiri+ na mavuno ya ngano yalipofikia mwisho. Naye akaendelea kukaa na mama-mkwe wake.+

3 Basi Naomi mama-mkwe wake akamwambia: “Binti yangu, je, sipaswi kukutafutia mahali pa kupumzika,+ ili mambo yapate kukuendea vema? 2 Basi sasa, je, Boazi, ambaye ulikuwa na wanawake wake vijana, si mtu wa ukoo wetu?+ Tazama! Usiku wa leo anapepeta+ shayiri kwenye uwanja wa kupuria. 3 Oga basi, ujipake mafuta,+ uvae nguo yako ya kujitanda,+ na uende mpaka kwenye uwanja wa kupuria. Usijitambulishe kwake mpaka amalize kula na kunywa. 4 Atakapolala, uangalie mahali ambapo atalala; uende ukamfunue miguuni pake, ulale hapo; naye atakuambia jambo utakalofanya.”

5 Basi akamwambia: “Yote ambayo umeniambia nitafanya.” 6 Naye akaenda kwenye uwanja wa kupuria na kufanya yote ambayo mama-mkwe wake alikuwa amemwamuru. 7 Basi Boazi akala na kunywa, nao moyo wake ukachangamka.+ Kisha akaenda kulala mwishoni mwa rundo la nafaka. Kisha Ruthu akaja kisirisiri akamfunua miguuni pake, akalala. 8 Ilipofika usiku wa manane mwanamume huyo akashtuka. Akageuka, na, tazama! mwanamke alikuwa amelala miguuni pake! 9 Ndipo akauliza: “Wewe ni nani?” Naye akajibu: “Mimi ni Ruthu kijakazi wako, basi mfunike kijakazi wako kwa upindo wa nguo yako, kwa maana wewe ni mkombozi.”+ 10 Basi Boazi akasema: “Yehova na akubariki,+ binti yangu. Umeonyesha fadhili zako zenye upendo+ kwa njia bora zaidi mara hii ya mwisho kuliko mara ya kwanza.+ Hukuwafuata vijana, wawe ni wa hali ya chini au matajiri. 11 Basi sasa, binti yangu, usiogope. Yote utakayosema nitakufanyia,+ kwa maana kila mtu aliye katika lango la watu wangu anajua kwamba wewe ni mwanamke bora sana.+ 12 Na sasa ingawa ni kweli kwamba mimi ni mkombozi,+ pia kuna mkombozi aliye wa jamaa ya karibu kuliko mimi.+ 13 Lala hapa usiku wa leo, na asubuhi ikiwa atakukomboa,+ sawa! Basi na akukomboe. Lakini asipotaka kukukomboa, nitakukomboa, mimi mwenyewe, kama anavyoishi Yehova.+ Endelea kulala mpaka asubuhi.”

14 Naye akalala miguuni pake mpaka asubuhi kisha akaamka kabla yeyote hajaweza kumtambua mwingine. Ndipo Boazi akasema: “Usiache ijulikane kwamba mwanamke alikuja kwenye uwanja wa kupuria.”+ 15 Naye akaendelea kusema: “Ulete ushungi ambao umevaa, uutandaze.” Basi Ruthu akautandaza, naye Boazi akampimia vipimo sita vya shayiri na kumtwika, kisha akaenda jijini.

16 Ruthu akaondoka na kuenda kwa mama-mkwe wake, ambaye alimuuliza: “Wewe ni nani, binti yangu?” Ndipo akamwambia kila kitu ambacho mwanamume huyo alikuwa amemfanyia. 17 Kisha akasema: “Vipimo hivi sita vya shayiri alinipa, kwa maana aliniambia, ‘Usiende mikono mitupu kwa mama-mkwe wako.’”+ 18 Basi Naomi akamwambia: “Keti utulie, binti yangu, mpaka utakapojua jinsi jambo hilo litakavyokuwa, kwa maana mwanamume huyo hatapumzika mpaka amalize jambo hilo leo.”+

4 Naye Boazi akaenda langoni+ na kuketi hapo. Na, tazama! yule mkombozi ambaye Boazi alikuwa amemtaja+ alikuwa akipita. Basi akasema: “Njoo, keti hapa, Fulani wa Fulani.” Basi akaja na kuketi. 2 Kisha akawachukua wanaume kumi kati ya wazee+ wa jiji akasema: “Ketini hapa.” Nao wakaketi.

3 Ndipo akamwambia mkombozi+ huyo: “Naomi aliyerudi kutoka katika uwanda wa Moabu+ atauza ile sehemu ya shamba lililokuwa la ndugu yetu Elimeleki.+ 4 Nilifikiri kwamba ninapaswa kukufunulia, nikuambie, ‘Linunue+ mbele ya wakaaji na wanaume wazee wa watu wangu.+ Ikiwa utalikomboa, likomboe; lakini ikiwa hutalikomboa, niambie, nipate kujua, kwa maana hakuna mwingine yeyote ila wewe wa kulikomboa,+ nami ninakufuata.’” Kisha akasema: “Mimi ndiye nitakayelikomboa.”+ 5 Halafu Boazi akasema: “Siku utakayolinunua shamba hilo mkononi mwa Naomi, utalinunua pia kutoka kwa Ruthu Mmoabu, mke wa mwanamume aliyekufa, ili umwinulie jina mwanamume huyo katika urithi wake.”+ 6 Basi mkombozi huyo akasema: “Mimi siwezi kukomboa, nisije nikaharibu urithi wangu mwenyewe. Wewe likomboe kwa kutumia haki yangu, kwa sababu mimi siwezi.”

7 Ili kuhakikisha jambo la kila namna, hii ndiyo iliyokuwa desturi ya nyakati za zamani katika Israeli kuhusu haki ya kukomboa na kuhusu mabadilishano: Mwanamume alipaswa kuvua kiatu+ chake na kumpa mwenzake, na huo ndio uliokuwa ushuhuda katika Israeli. 8 Kwa hiyo mkombozi huyo alipomwambia Boazi: “Kinunue kiwe chako,” akavua kiatu chake.+ 9 Kisha Boazi akawaambia wanaume wazee na watu wote: “Ninyi ni mashahidi+ leo kwamba ninanunua vyote vilivyokuwa vya Elimeleki na vyote vilivyokuwa vya Kilioni na Maloni mkononi mwa Naomi. 10 Na pia Ruthu Mmoabu, mke wa Maloni, ninamnunua awe mke wangu ili nimwinulie mwanamume aliyekufa+ jina katika urithi wake na kwamba jina la mwanamume aliyekufa lisipate kukatiliwa mbali kati ya ndugu zake na katika lango la mahali pake. Ninyi ni mashahidi+ leo.”

11 Basi watu wote waliokuwa katika lango hilo na wale wanaume wazee wakasema: “Sisi ni mashahidi! Yehova na amwezeshe mke anayekuja nyumbani mwako kuwa kama Raheli+ na kama Lea,+ wale wawili walioijenga nyumba ya Israeli;+ nawe uhakikishe thamani yako katika Efratha+ na kufanya jina lenye sifa katika Bethlehemu.+ 12 Nyumba yako na iwe kama nyumba ya Perezi, ambaye Tamari alimzalia Yuda,+ kutokana na uzao ambao Yehova atakupa kutoka kwa huyu mwanamke kijana.”+

13 Basi Boazi akamchukua Ruthu naye akawa mke wake, akalala naye. Yehova akamwezesha kupata mimba+ naye akazaa mwana. 14 Nao wanawake wakaanza kumwambia+ Naomi: “Na abarikiwe Yehova,+ ambaye amehakikisha kwamba mtu wa kukukomboa hakukosekana leo; jina lake na lipate kutangazwa katika Israeli. 15 Naye atakurudishia nafsi yako na kukutunza katika uzee+ wako, kwa sababu binti-mkwe wako anayekupenda,+ ambaye ni bora kwako kuliko wana saba,+ amemzaa huyo.” 16 Naye Naomi akamchukua huyo mtoto, akamweka kifuani pake, akawa mlezi wake. 17 Kisha wanawake majirani+ wakampa jina, wakisema: “Naomi amepata mwana.” Nao wakamwita Obedi.+ Yeye ndiye baba ya Yese,+ baba ya Daudi.

18 Basi hivi ndivyo vizazi vya Perezi:+ Perezi akamzaa Hezroni;+ 19 na Hezroni akamzaa Ramu; na Ramu+ akamzaa Aminadabu; 20 na Aminadabu+ akamzaa Nashoni;+ na Nashoni akamzaa Salmoni; 21 na Salmoni+ akamzaa Boazi; na Boazi+ akamzaa Obedi; 22 na Obedi akamzaa Yese;+ na Yese akamzaa Daudi.+

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki