Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt Amosi 1:1-9:15
  • Amosi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Amosi
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Amosi

AMOSI

1 Maneno ya Amosi,* aliyekuwa mmoja wa wafugaji wa kondoo kutoka Tekoa,+ aliyoyapokea katika maono kuhusu Israeli katika siku za utawala wa Mfalme Uzia+ wa Yuda na katika siku za utawala wa Yeroboamu+ mwana wa Yoashi,+ mfalme wa Israeli, miaka miwili kabla ya tetemeko la ardhi.+ 2 Alisema:

“Yehova atanguruma kutoka Sayuni,

Naye atapaza sauti yake kutoka Yerusalemu.

Malisho ya wachungaji yataomboleza,

Na kilele cha Karmeli kitakauka.”+

 3 “Yehova anasema hivi:

‘“Kwa sababu ya maasi matatu* ya Damasko, na hata manne, sitabadili uamuzi wangu,

Kwa sababu walipura Gileadi kwa vifaa vya chuma vya kupuria.+

 4 Kwa hiyo nitaishushia moto nyumba ya Hazaeli,+

Nao utateketeza kabisa minara ya Ben-hadadi yenye ngome.+

 5 Nitavunja makomeo ya Damasko;+

Nitawaangamiza wakaaji wa Bikath-aveni

Na yule anayetawala* Beth-edeni;

Na watu wa Siria watapelekwa uhamishoni kule Kiri,”+ asema Yehova.’

 6 Yehova anasema hivi:

‘“Kwa sababu ya maasi matatu ya Gaza,+ na hata manne, sitabadili uamuzi wangu,

Kwa sababu walichukua kundi lote la mateka+ na kuwatia mikononi mwa Edomu.

 7 Basi nitaushushia moto ukuta wa Gaza,+

Nao utateketeza kabisa minara yake yenye ngome.

 8 Nitawaangamiza wakaaji wa Ashdodi,+

Na mtawala* wa Ashkeloni;+

Nitaugeuza mkono wangu dhidi ya Ekroni,+

Na Wafilisti wanaobaki wataangamia,”+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.’

 9 Yehova anasema hivi:

‘Kwa sababu ya maasi matatu ya Tiro,+ na hata manne, sitabadili uamuzi wangu,

Kwa sababu walilitia mikononi mwa Edomu kundi lote la watu waliohamishwa,

Na kwa sababu hawakukumbuka agano la ndugu.+

10 Basi nitaushushia moto ukuta wa Tiro,

Nao utateketeza kabisa minara yake yenye ngome.’+

11 Yehova anasema hivi:

‘Kwa sababu ya maasi matatu ya Edomu,+ na hata manne, sitabadili uamuzi wangu,

Kwa sababu alimfuatia kwa upanga ndugu yake mwenyewe,+

Na kwa sababu alikataa kuonyesha rehema;

Katika hasira yake anaendelea kuwararuararua bila huruma,

Na bado anaendelea kuwakasirikia vikali.+

12 Basi nitaishushia moto Temani,+

Nao utateketeza kabisa minara ya Bosra yenye ngome.’+

13 Yehova anasema hivi:

‘“Kwa sababu ya maasi matatu ya Waamoni,+ na hata manne, sitabadili uamuzi wangu,

Kwa sababu waliwapasua tumbo wanawake wenye mimba wa Gileadi ili wapanue eneo lao wenyewe.+

14 Basi nitaushushia moto ukuta wa Raba,+

Nao utateketeza kabisa ngome zake zenye minara,

Kwa kelele za vita katika siku ya mapigano,

Kwa tufani katika siku ya kimbunga.

15 Na mfalme wao atapelekwa uhamishoni pamoja na wakuu wake,”+ asema Yehova.’

2 “Yehova anasema hivi:

‘“Kwa sababu ya maasi matatu* ya Moabu,+ na hata manne, sitabadili uamuzi wangu,

Kwa sababu aliiteketeza mifupa ya mfalme wa Edomu kwa ajili ya chokaa.

 2 Kwa hiyo nitaishushia moto Moabu,

Nao utateketeza kabisa minara ya Keriothi yenye ngome;+

Moabu itakufa katika ghasia,

Kwa kelele za vita, kwa mlio wa pembe.+

 3 Nitamwondoa mtawala* miongoni mwake

Na kuwaua wakuu wake wote pamoja naye,”+ asema Yehova.’

 4 Yehova anasema hivi:

‘Kwa sababu ya maasi matatu ya Yuda,+ na hata manne, sitabadili uamuzi wangu,

Kwa sababu walikataa sheria* ya Yehova,

Na kwa sababu hawakufuata masharti yake;+

Lakini uwongo uleule ambao mababu zao walifuata umewapotosha.+

 5 Kwa hiyo nitaishushia moto Yuda,

Nao utateketeza kabisa minara ya Yerusalemu yenye ngome.’+

 6 Yehova anasema hivi:

‘Kwa sababu ya maasi matatu ya Israeli,+ na hata manne, sitabadili uamuzi wangu,

Kwa sababu wanamuuza mwadilifu ili wapate fedha,

Na maskini kwa jozi ya viatu.+

 7 Wanavikanyaga-kanyaga vichwa vya watu wa hali ya chini katika mavumbi ya dunia,+

Nao wanaziba njia ya wapole.+

Mtu na baba yake wanalala na msichana yuleyule,

Na hivyo kulichafua jina langu takatifu.

 8 Wanajinyoosha kando ya kila madhabahu+ juu ya nguo walizochukua kwa nguvu kutoka kwa maskini kama dhamana ya mkopo;*+

Na divai wanayokunywa katika nyumba ya* miungu yao waliipata kutoka kwa wale waliowatoza faini.’

 9 ‘Lakini ni mimi niliyemwangamiza Mwamori mbele yao,+

Aliyekuwa mrefu kama mierezi na mwenye nguvu kama mialoni;

Niliyaharibu matunda yake juu na mizizi yake chini.+

10 Nilikupandisha kutoka nchini Misri,+

Nami nikakufanya utembee kupitia nyikani kwa miaka 40,+

Ili umiliki nchi ya Mwamori.

11 Niliwainua baadhi ya wana wako kuwa manabii+

Na baadhi ya vijana wako wa kiume kuwa Wanadhiri.+

Je, sivyo ilivyo, enyi watu wa Israeli?’ asema Yehova.

12 ‘Lakini uliendelea kuwapa Wanadhiri divai wanywe,+

Nawe ukawaamuru hivi manabii: “Hampaswi kutoa unabii.”+

13 Basi nitakupondaponda mahali pako,

Kama vile ambavyo gari la kukokotwa lililojazwa miganda ya nafaka iliyotoka kuvunwa linavyopondaponda kilicho njiani.

14 Mwenye mbio hatakuwa na mahali pa kukimbilia,+

Mwenye nguvu hatabaki na nguvu zake,

Na hakuna shujaa atakayeokoa uhai wake.*

15 Mwanamume anayeshika upinde hatasimama,

Mtu anayekimbia kwa kasi* hataponyoka,

Na mpanda farasi hataokoa uhai wake.*

16 Hata mashujaa wenye ujasiri* zaidi

Watakimbia uchi siku hiyo,’+ asema Yehova.”

3 “Sikieni neno hili ambalo Yehova amesema kuwahusu ninyi, enyi watu wa Israeli, kuhusu familia nzima niliyoipandisha kutoka nchini Misri:

 2 ‘Ni ninyi peke yenu niliowajua kati ya familia zote duniani.+

Ndiyo sababu nitawafanya muwajibike* kwa sababu ya makosa yenu yote.+

 3 Je, watu wawili watatembea pamoja ikiwa hawajakubaliana kukutana?*

 4 Je, simba atanguruma mwituni ikiwa hana mawindo?

Je, mwanasimba* atanguruma pangoni mwake ikiwa hajakamata chochote?

 5 Je, ndege ataanguka kwenye mtego ardhini ikiwa hakuna mtego wa kumnasa?*

Je, mtego hufyatuka ardhini ikiwa haujanasa chochote?

 6 Pembe ikipigwa jijini, je, watu hawatetemeki?

Msiba ukitokea jijini, je, si Yehova aliyetenda?

 7 Kwa maana Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hatafanya jambo lolote

Kabla hajawafunulia watumishi wake manabii siri yake.+

 8 Simba amenguruma!+ Ni nani ambaye hataogopa?

Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova amesema! Ni nani ambaye hatatoa unabii?’+

 9 ‘Tangazeni jambo hilo kwenye minara ya Ashdodi yenye ngome

Na kwenye minara yenye ngome katika nchi ya Misri.

Semeni: “Kusanyikeni pamoja dhidi ya milima ya Samaria;+

Tazameni machafuko yaliyo ndani yake

Na ulaghai ulio ndani yake.+

10 Kwa maana hawajui kufanya yaliyo sawa,” asema Yehova,

“Wale wanaojikusanyia ukatili na maangamizi katika minara yao yenye ngome.”’

11 Kwa hiyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi:

‘Adui ataizingira nchi,+

Atakuvua nguvu zako,

Na minara yako yenye ngome itaporwa.’+

12 Yehova anasema hivi:

‘Kama mchungaji anavyompokonya simba miguu miwili au kipande cha sikio kutoka kinywani mwake,

Hivyo ndivyo watu wa Israeli watakavyookolewa,

Wale ambao sasa wanaketi kwenye vitanda vya kifahari na kwenye makochi bora* kule Samaria.’+

13 ‘Sikieni na kuionya* nyumba ya Yakobo,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, Mungu wa majeshi.

14 ‘Kwa maana siku nitakapowafanya Waisraeli wawajibike* kwa sababu ya maasi yao yote,*+

Pia nitawafanya wawajibike kwa sababu ya madhabahu za Betheli;+

Pembe za madhabahu zitakatwa na kuanguka ardhini.+

15 Nitaibomoa nyumba ya majira ya baridi kali pamoja na nyumba ya majira ya kiangazi.’

‘Nyumba za pembe za tembo zitatoweka,+

Na majumba makubwa hayatasalia,’*+ asema Yehova.”

4 “Sikieni neno hili, enyi ng’ombe wa Bashani,

Mlio kwenye mlima wa Samaria,+

Ninyi wanawake mnaowalaghai watu wa hali ya chini+ na kuwakandamiza maskini,

Mnaowaambia waume zenu,* ‘Tuleteeni kinywaji!’

 2 Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova ameapa kwa utakatifu wake,

‘“Tazameni! Siku zinakuja wakati ambapo atawainua juu kwa kulabu za mchinjaji wa wanyama

Na wale watakaobaki kati yenu kwa ndoano za samaki.

 3 Kila mmoja wenu atatoka nje moja kwa moja kupitia sehemu zilizobomolewa ukutani;

Nanyi mtatupwa kule Harmoni,” asema Yehova.’

 4 ‘Njooni Betheli mtende dhambi,*+

Njooni Gilgali mzidi kutenda dhambi!+

Leteni dhabihu zenu+ asubuhi,

Na sehemu zenu za kumi+ katika siku ya tatu.

 5 Teketezeni dhabihu ya shukrani ya mikate iliyotiwa chachu;+

Tangazeni kwa sauti matoleo yenu ya hiari!

Kwa maana hivyo ndivyo mnavyopenda kufanya, enyi watu wa Israeli,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.

 6 ‘Lakini mimi niliyafanya meno yenu yawe safi bila chakula* katika majiji yenu yote

Nikasababisha mkose mikate katika nyumba zenu zote;+

Lakini hamkunirudia,’+ asema Yehova.

 7 ‘Pia niliwanyima mvua miezi mitatu kabla ya mavuno;+

Nilileta mvua katika jiji moja lakini sikuileta katika jiji lingine.

Shamba moja lilipata mvua,

Lakini shamba lingine lilikauka kwa sababu halikupata mvua.

 8 Watu wa majiji mawili au matatu walipepesuka kwenda kwenye jiji moja kunywa maji,+

Nao hawakutosheka;

Lakini hamkunirudia,’+ asema Yehova.

 9 ‘Niliwapiga kwa joto linalounguza na kuvu.+

Mlizidisha bustani zenu na mashamba yenu ya mizabibu,

Lakini nzige walitafuna mitini yenu na mizeituni yenu;+

Na bado hamkunirudia,’+ asema Yehova.

10 ‘Niliwaletea ugonjwa hatari kama ule wa* Misri.+

Niliwaua vijana wenu wa kiume+ kwa upanga na kuwateka farasi wenu.+

Nilifanya uvundo wa kambi zenu upande katika mianzi ya pua zenu;+

Lakini hamkunirudia,’ asema Yehova.

11 ‘Niliwaangamiza

Kama Mungu alivyoangamiza Sodoma na Gomora.+

Nanyi mlikuwa kama gogo lililochomolewa haraka motoni;

Lakini hamkunirudia,’+ asema Yehova.

12 Basi hivyo ndivyo nitakavyokutendea, Ee Israeli.

Kwa kuwa nitakutendea hivyo,

Jitayarishe kukutana na Mungu wako, Ee Israeli.

13 Kwa maana tazama! yeye Ndiye aliyeumba milima+ na kuumba upepo;+

Humwambia mwanadamu mawazo Yake,

Hubadili mapambazuko kuwa giza,+

Naye hukanyaga vilele vya dunia;+

Yehova Mungu wa majeshi ndilo jina lake.”

5 “Sikieni neno hili ninalosema dhidi yenu kama wimbo wa huzuni,* Ee nyumba ya Israeli:

 2 ‘Bikira, Israeli, ameanguka;

Hawezi kuinuka tena.

Ameachwa peke yake katika ardhi yake mwenyewe;

Hakuna yeyote wa kumwinua.’

3 “Kwa maana Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi:

‘Jiji linaloenda vitani likiwa na watu elfu moja litabaki na watu mia moja;

Na lile linaloenda vitani na watu mia moja litabaki na watu kumi, hili linahusu nyumba ya Israeli.’+

4 “Kwa maana Yehova anaiambia hivi nyumba ya Israeli:

‘Nitafuteni mimi mwendelee kuishi.+

 5 Msitafute Betheli,+

Msiende Gilgali+ wala msivuke kwenda Beer-sheba,+

Kwa maana Gilgali hakika litapelekwa uhamishoni,+

Na Betheli litaangamizwa.*

 6 Mtafuteni Yehova, mwendelee kuishi,+

Ili asilipuke kama moto kwenye nyumba ya Yosefu,

Na kuteketeza kabisa Betheli, hivi kwamba hakuna mtu atakayeweza kuuzima moto huo.

 7 Mnabadili haki kuwa pakanga,*

Nanyi mnautupa uadilifu ardhini.+

 8 Yule aliyeumba kundi la nyota la Kima* na kundi la nyota la Kesili,*+

Yule anayebadili kivuli kizito kuwa asubuhi,

Yule anayefanya mchana uwe na giza kama usiku,+

Yule anayeyaita maji ya bahari

Ili ayamwage kwenye nchi kavu+

—Yehova ndilo jina lake.

 9 Atasababisha maangamizi yawajie kwa ghafla wenye nguvu,

Na kuharibu ngome.

10 Wanawachukia wale wanaotoa karipio kwenye lango la jiji,

Na kuwachukia sana watu wanaosema ukweli.+

11 Kwa sababu mnamdai maskini kodi ya* shamba

Nanyi mnachukua nafaka yake kama ushuru,+

Hamtaendelea kuishi katika nyumba mlizojenga kwa mawe yaliyochongwa+

Wala hamtakunywa divai kutoka katika mashamba bora ya mizabibu mliyopanda.+

12 Kwa maana ninajua jinsi maasi yenu* yalivyo mengi

Na jinsi dhambi zenu zilivyo kubwa

—Mnawanyanyasa waadilifu,

Mnapokea rushwa,*

Nanyi mnawanyima maskini haki zao kwenye lango la jiji.+

13 Kwa hiyo, wale walio na ufahamu watanyamaza kimya wakati huo,

Kwa sababu utakuwa wakati wa msiba.+

14 Tafuteni yaliyo mema, na wala si maovu,+

Ili mwendelee kuishi.+

Ndipo huenda Yehova Mungu wa majeshi atakuwa pamoja nanyi,

Kama mnavyosema yuko pamoja nanyi.+

15 Chukieni maovu, pendeni yaliyo mema,+

Acheni haki itawale kwenye lango la jiji.+

Huenda Yehova Mungu wa majeshi

Atawaonyesha kibali wazao waliobaki wa Yosefu.’+

16 “Kwa hiyo Yehova Mungu wa majeshi, Yehova, anasema hivi:

‘Watu watalia kwa sauti katika viwanja vyote vya jiji,

Katika barabara zote watasema, “Ole! Ole!”

Watawaita wakulima waomboleze

Na waombolezaji wa kulipwa walie kwa sauti.’

17 ‘Kutakuwa na kilio katika kila shamba la mizabibu;+

Kwa maana nitapita katikati yenu,’ asema Yehova.

18 ‘Ole wao wanaoitamani siku ya Yehova!+

Basi, siku ya Yehova itamaanisha nini kwenu?+

Itakuwa giza, wala si nuru.+

19 Itakuwa kama mtu anayemkimbia simba, kisha anakutana na dubu,

Na anapoingia nyumbani mwake na kuuegemeza mkono wake ukutani, anaumwa na nyoka.

20 Je, siku ya Yehova haitakuwa giza, wala si nuru;

Je, haitakuwa na utusitusi, wala si mwangaza?

21 Nazichukia, nazidharau sherehe zenu,+

Nami sifurahii harufu tamu ya makusanyiko yenu matakatifu.

22 Hata mkinitolea dhabihu nzima za kuteketezwa na matoleo ya zawadi,

Sitazifurahia;+

Nami sitapendezwa na dhabihu zenu za ushirika za wanyama waliononeshwa.+

23 Niondoleeni kelele za nyimbo zenu;

Na sitaki kusikia miziki ya vinanda vyenu.+

24 Acheni haki itiririke kama maji,+

Na uadilifu kama kijito kinachotiririka daima.

25 Je, uliniletea dhabihu na matoleo ya zawadi

Kwa miaka 40 uliyokuwa nyikani, Ee nyumba ya Israeli?+

26 Sasa mtalazimika kumchukua Sakuthi mfalme wenu na Kaiwani,*

Sanamu zenu, nyota ya mungu wenu ambaye mlijitengenezea,

27 Nami nitawapeleka uhamishoni mbali kupita Damasko,’+ anasema yeye ambaye jina lake ni Yehova Mungu wa majeshi.”+

6 “Ole wao wanaojitumaini* huko Sayuni,

Wale wanaojiona wakiwa salama katika mlima wa Samaria,+

Wanaume maarufu wa taifa kuu zaidi kati ya mataifa,

Wale ambao nyumba ya Israeli huwaendea!

 2 Vukeni mwende Kalne mkaone.

Tokeni huko mwende katika Jiji Kubwa la Hamathi,+

Na mteremke mpaka jiji la Gathi la Wafilisti.

Je, majiji hayo ni bora kuliko falme hizi,*

Au je, eneo lao ni kubwa kuliko lenu?

 3 Je, mnaiondoa akilini mwenu ile siku ya msiba+

Na kuukaribisha utawala wa* ukatili?+

 4 Wanalalia vitanda vya pembe za tembo+ na kujinyoosha kwenye makochi,+

Wakila kondoo dume wa kundi na ndama* waliononeshwa;+

 5 Wanatunga nyimbo papo hapo kupatana na sauti ya kinubi,*+

Na kama Daudi, wanabuni ala za muziki;+

 6 Wanakunywa divai iliyojazwa kwenye mabakuli+

Na kujitia wenyewe mafuta yaliyo bora.

Lakini hawajali* msiba wa Yosefu.+

 7 Basi watakuwa mstari wa mbele kupelekwa uhamishoni,+

Na karamu zenye shamrashamra za wanaojinyoosha kwa starehe zitakoma.

 8 ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova ameapa kwa nafsi yake mwenyewe,’+ asema Yehova Mungu wa majeshi,

‘“Nakichukia sana kiburi cha Yakobo,+

Naichukia minara yake yenye ngome,+

Nami nitawapa wengine jiji lao na vyote vilivyomo.+

9 “‘“Na watu kumi wakibaki katika nyumba moja, wao pia watakufa. 10 Mtu wa ukoo* atakuja na kuwatoa nje na kuwachoma mmoja baada ya mwingine. Ataitoa mifupa yao ndani ya nyumba hiyo; kisha atamuuliza yeyote aliye katika vyumba vya ndani vya nyumba hiyo, ‘Je, kuna wengine pamoja nawe?’ Naye atajibu, ‘Hakuna yeyote!’ Kisha atasema, ‘Nyamaza kimya! Kwa maana huu si wakati wa kutaja kwa vyovyote vile jina la Yehova.’”

11 Kwa maana ni Yehova anayetoa amri hiyo,+

Naye ataibomoa ile nyumba kubwa ibaki rundo la mawe,

Na nyumba ndogo ibaki kifusi.+

12 Je, farasi hukimbia kwenye mwamba,

Au je, mtu anaweza kulima kwa ng’ombe kwenye mwamba?

Kwa maana mmebadili haki kuwa mmea wenye sumu,

Na tunda la uadilifu kuwa pakanga.*+

13 Mnashangilia jambo lisilo na manufaa yoyote,

Nanyi mnasema, “Je, hatujapata nguvu* kwa uwezo wetu wenyewe?”+

14 Kwa hiyo, Ee nyumba ya Israeli, nitaleta taifa dhidi yenu,’+ asema Yehova Mungu wa majeshi,

‘Nao litawakandamiza kuanzia Lebo-hamathi*+ mpaka kwenye Korongo* la Araba.’”

7 Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova alinionyesha mambo haya: Tazama! Alileta kundi la nzige mimea ya mwisho* ilipokuwa ikianza kuchipuka. Mimea hiyo ilipandwa baada ya nyasi za mfalme kukatwa. 2 Kundi hilo la nzige lilipomaliza kula mimea nchini, nikasema: “Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, tafadhali samehe!+ Yakobo ataendeleaje kuishi?* Kwa maana yuko dhaifu!”+

3 Basi Yehova akafikiria upya* jambo hilo.+ Yehova akasema, “Hilo halitatokea.”

4 Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova alinionyesha mambo haya: Tazama! Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova aliamuru moto uje kuwaadhibu. Ukateketeza vilindi vikubwa vya maji, na kuteketeza sehemu ya nchi. 5 Kisha nikasema: “Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, tafadhali lizuie jambo hili lisitendeke.+ Yakobo ataendeleaje kuishi?* Kwa maana yuko dhaifu!”+

6 Basi Yehova akafikiria upya* jambo hilo.+ Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova akasema, “Hilo pia halitatokea.”

7 Alinionyesha mambo haya: Tazama! Yehova alikuwa amesimama juu ya ukuta uliojengwa kwa timazi,* na timazi ilikuwa mkononi mwake. 8 Kisha Yehova akaniuliza: “Unaona nini, Amosi?” Nikamjibu: “Timazi.” Ndipo Yehova akasema: “Tazama naweka timazi kati ya watu wangu Waisraeli. Sitawasamehe tena.+ 9 Sehemu za juu za Isaka+ zitaachwa ukiwa, na mahali patakatifu pa Waisraeli pataharibiwa kabisa;+ nami nitaishambulia nyumba ya Yeroboamu kwa upanga.”+

10 Kuhani Amazia wa Betheli+ akatuma ujumbe huu kwa Mfalme Yeroboamu+ wa Israeli: “Amosi anapanga njama dhidi yako katikati kabisa ya nyumba ya Israeli.+ Nchi haiwezi kuvumilia maneno yake yote.+ 11 Kwa maana Amosi anasema hivi: ‘Yeroboamu atauawa kwa upanga; na kwa hakika Waisraeli watapelekwa uhamishoni kutoka katika nchi yao.’”+

12 Kisha Amazia akamwambia Amosi: “Ee mwonaji, nenda, kimbia uende katika nchi ya Yuda, jitafutie mkate wako* huko, nawe unaweza kutoa unabii wako huko.+ 13 Lakini usiendelee kutoa unabii hapa Betheli,+ kwa maana ni mahali patakatifu pa mfalme+ na nyumba ya ufalme.”

14 Ndipo Amosi akamjibu hivi Amazia: “Mimi sikuwa nabii wala mwana wa nabii; bali nilikuwa mchungaji wa mifugo,+ nami nilitunza mitini ya mikuyu.* 15 Lakini Yehova aliniondoa katika kazi ya kuchunga kundi, kisha Yehova akaniambia, ‘Nenda, toa unabii kwa watu wangu Waisraeli.’+ 16 Basi sasa sikia neno la Yehova: ‘Wewe unasema: “Usitoe unabii dhidi ya Israeli,+ na usihubiri+ dhidi ya nyumba ya Isaka.” 17 Kwa hiyo Yehova anasema hivi: “Mke wako atakuwa kahaba jijini, na wana wako na mabinti wako watauawa kwa upanga. Ardhi yako itagawanywa kwa wengine kwa kamba ya kupimia, na wewe mwenyewe utafia katika nchi isiyo safi; na kwa hakika Waisraeli watapelekwa uhamishoni kutoka katika nchi yao.”’”+

8 Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova alinionyesha mambo haya: Tazama! Kulikuwa na kikapu chenye matunda ya wakati wa kiangazi. 2 Kisha akaniuliza, “Unaona nini, Amosi?” Nikajibu, “Kikapu chenye matunda ya wakati wa kiangazi.” Kisha Yehova akaniambia: “Mwisho wa watu wangu Waisraeli umefika. Sitawasamehe tena.+ 3 ‘Siku hiyo nyimbo za hekalu zitabadilika kuwa kilio kikubwa,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. ‘Kutakuwa na mizoga mingi iliyotupwa kila mahali+—kimya cha ajabu!’

 4 Sikieni hili, ninyi mnaowakandamiza maskini

Na kuwaangamiza wapole nchini,+

 5 Mnaosema, ‘Sherehe ya mwezi mpya itakwisha lini,+ ili tuuze nafaka yetu,

Na Sabato+ itakwisha lini, tukauze nafaka?

Ili tupunguze kipimo cha efa*

Na kuongeza uzito wa shekeli,*

Kuipotosha mizani yetu ya udanganyifu;+

 6 Ili tuwanunue wenye uhitaji kwa fedha

Na maskini kwa jozi ya viatu,+

Na kuuza makapi ya nafaka.’

 7 Yehova ameapa kwa Fahari ya Yakobo,+

‘Sitasahau kamwe matendo yao yote.+

 8 Kwa sababu hiyo nchi* itatetemeka,

Na kila mkaaji nchini ataomboleza.+

Je, nchi yote haitapanda kama Mto Nile,

Na kuinuka na kushuka chini kama Mto Nile wa Misri?’+

 9 ‘Siku hiyo,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova,

‘Nitalifanya jua litue wakati wa adhuhuri,

Nami nitaitia nchi giza siku nyangavu.+

10 Nitabadili sherehe zenu ziwe maombolezo+

Na nyimbo zenu zote ziwe nyimbo za huzuni.*

Nitavisha nyonga zote nguo za magunia na kukitia kila kichwa upara;

Nitafanya wakati huo uwe kama wakati wa kumwombolezea mwana wa pekee,

Na mwisho wake kama siku yenye uchungu.’

11 ‘Tazama! Siku zinakuja,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova,

‘Nitakapoleta njaa kali nchini,

Si njaa kali ya chakula* au kiu ya maji,

Bali ya kusikia maneno ya Yehova.+

12 Watapepesuka kutoka bahari mpaka bahari

Na kutoka kaskazini mpaka mashariki.*

Watatangatanga wakitafuta neno la Yehova, lakini hawatalipata.

13 Siku hiyo mabikira warembo watazimia,

Na pia vijana wa kiume, kwa sababu ya kiu;

14 Wale wanaoapa kwa hatia ya Samaria+ na kusema,

“Kwa hakika kama mungu wako anavyoishi, Ee Dani!”+

Na, “Kwa hakika kama inavyoishi njia ya Beer-sheba!”+

Wataanguka, na hawatainuka tena.’”+

9 Nilimwona Yehova+ akiwa juu ya madhabahu, naye akasema: “Piga kichwa cha nguzo, na vizingiti vitatikisika. Kata vichwa vya nguzo, nami nitamuua wa mwisho kwa upanga. Hakuna yeyote anayekimbia atakayeponyoka, na hakuna yeyote anayejaribu kutoroka atakayefanikiwa.+

 2 Wakichimba chini kuingia Kaburini,*

Mkono wangu utawatoa humo;

Na wakipanda juu mbinguni,

Nitawashusha chini kutoka huko.

 3 Nao wakijificha kwenye kilele cha Karmeli,

Nitawasaka na kuwatoa huko.+

Wakijificha chini ya bahari ili macho yangu yasiwaone,

Huko nitamwamuru nyoka awaume.

 4 Wakipelekwa utekwani na maadui wao,

Huko nitauamuru upanga, nao utawaua;+

Nitawakazia macho kwa mabaya, wala si kwa mema.+

 5 Kwa maana Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova wa majeshi, Ndiye anayeigusa nchi,*

Hivi kwamba inayeyuka,+ na wakaaji wake wote wataomboleza;+

Na nchi yote itapanda kama Mto Nile,

Na kushuka chini kama Mto Nile wa Misri.+

 6 ‘Yule anayejenga ngazi zake mbinguni

Na kujenga jengo* lake juu ya dunia;

Yule anayeyaita maji ya bahari,

Ili ayamwage duniani+

—Yehova ndilo jina lake.’+

 7 ‘Je, ninyi si kama wana wa Wakushi kwangu, enyi watu wa Israeli?’ asema Yehova.

‘Je, sikuwapandisha Waisraeli kutoka nchini Misri,+

Na Wafilisti kutoka Krete,+ na Wasiria kutoka Kiri?’+

 8 ‘Tazameni! Macho ya Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova yanautazama ufalme huu wenye dhambi,

Naye atauangamiza kabisa kutoka nchini.+

Lakini sitaiangamiza kabisa nyumba ya Yakobo,’+ asema Yehova.

 9 ‘Kwa maana tazameni! Ninatoa amri,

Nami nitaichekecha nyumba ya Israeli miongoni mwa mataifa yote,+

Kama mtu anavyochekecha nafaka kwa chujio,

Na hakuna kijiwe hata kimoja kinachoanguka chini.

10 Watu wangu wote wanaotenda dhambi watauawa kwa upanga,

Wale wanaosema: “Msiba hautatukaribia wala kutufikia.”’

11 ‘Siku hiyo nitakiinua kibanda cha Daudi+ kilichoanguka,*

Nitarekebisha sehemu* zilizoharibika,

Na kujenga upya magofu yake;

Nitakijenga upya kama kilivyokuwa siku za kale,+

12 Ili wamiliki sehemu zilizobaki za Edomu,+

Na mataifa yote yanayoitwa kwa jina langu,’ asema Yehova, anayefanya hayo.

13 ‘Tazameni! Siku zinakuja,’ asema Yehova,

‘Wakati ambapo mtu anayelima kwa plau atampita anayevuna,

Na anayekanyaga zabibu atampita anayepanda mbegu;+

Na milima itadondosha divai tamu,+

Na vilima vyote vitatiririka divai.*+

14 Nitawakusanya na kuwarudisha watu wangu Waisraeli walio utekwani,+

Nao watajenga upya majiji yaliyoachwa ukiwa na kuishi humo;+

Watapanda mashamba ya mizabibu na kunywa divai yake,+

Nao watalima bustani za matunda na kula matunda yake.’+

15 ‘Nitawapanda katika nchi yao,

Nao hawatang’olewa tena kamwe

Kutoka katika nchi yao ambayo nimewapa,’+ asema Yehova Mungu wenu.”

Maana yake “Kuwa Mzigo” au “Kubeba Mzigo.”

Au “matendo matatu ya uhalifu.”

Tnn., “yule anayeshika fimbo ya ufalme.”

Tnn., “yule anayeshika fimbo ya ufalme.”

Au “matendo matatu ya uhalifu.”

Tnn., “mwamuzi.”

Au “mafundisho.”

Au “rehani.”

Au “hekalu la.”

Au “nafsi yake.”

Tnn., “mwenye miguu myepesi.”

Au “nafsi yake.”

Au “wenye moyo mkuu.”

Au “nitawaadhibu.”

Au “hawajakutana kama walivyokubaliana.”

Au “mwanasimba mwenye manyoya marefu shingoni.”

Au labda, “ikiwa hauna chambo?”

Au “makochi ya Damasko.”

Au “kutoa ushahidi dhidi ya.”

Au “nitakapowaadhibu Waisraeli.”

Au “matendo yao yote ya uhalifu.”

Au labda, “nyumba nyingi hazitasalia.”

Au “mabwana wenu wakubwa.”

Au “mfanye uasi.”

Au “sikuwapa chakula chochote.”

Au “tauni kama ile ya.”

Au “wimbo wa maombolezo.”

Au labda, “litakuwa kitu cha uchawi.”

Au “uchungu.”

Labda ni nyota zinazoitwa Pleiadesi katika kundi la nyota la Taurusi, au Ng’ombe.

Labda ni kundi la nyota la Orioni.

Au “ushuru wa.”

Au “matendo yenu ya uhalifu.”

Au “hongo.”

Huenda miungu hiyo miwili inarejelea sayari ya Zohali, ambayo iliabudiwa kama mungu.

Au “wasiojali.”

Inaonekana falme hizo ni Yuda na Israeli.

Tnn., “kukikaribisha kiti cha.”

Au “ng’ombe dume wachanga.”

Au “kinanda.”

Tnn., “hawakuwa wagonjwa kwa sababu ya.”

Tnn., “Ndugu ya baba yake.”

Au “uchungu.”

Tnn., “hatukujitwalia pembe.”

Au “njia ya kuingia Hamathi.”

Angalia Kamusi.

Yaani, mwezi wa Januari na Februari.

Tnn., “atainukaje?”

Au “akaghairi kuhusu.”

Tnn., “atainukaje?”

Au “akaghairi kuhusu.”

Au “chubwi; bildi.”

Au “kula mkate.”

Au “nilichanja tini za mikuyu.”

Angalia Nyongeza B14.

Angalia Nyongeza B14.

Au “dunia.”

Au “maombolezo.”

Tnn., “mkate.”

Au “mawio ya jua.”

Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.

Au “dunia.”

Au “kuba.”

Au “hema la Daudi lililoanguka.”

Au “sehemu zao.”

Tnn., “vitayeyuka.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki