Yoeli
1 Neno la Yehova lililomjia+ Yoeli mwana wa Pethueli:
2 “Sikieni jambo hili, ninyi wanaume wazee, tegeni sikio, ninyi wakaaji wote wa nchi.+ Je, hili limetokea katika siku zenu, au hata katika siku za mababu zenu?+ 3 Kuhusu hilo wasimulieni wana wenu wenyewe, nao wawasimulie wana wao, nao wana wao wasimulie kizazi kinachofuata.+ 4 Kilichoachwa na kiwavi, nzige amekula;+ kilichoachwa na nzige, nzige mchanga amekula; kilichoachwa na nzige mchanga, mende amekula.+
5 “Amkeni, ninyi walevi,+ lieni; pigeni mayowe,+ ninyi nyote wanywaji wa divai, kwa sababu ya divai tamu,+ kwa maana imekatiliwa mbali kutoka katika vinywa vyenu.+ 6 Kwa maana kuna taifa ambalo limeingia katika nchi yangu, lenye nguvu nalo halihesabiki.+ Meno yake ni meno ya simba,+ nalo lina mifupa ya mataya ya simba. 7 Limefanya mzabibu wangu kuwa kitu cha kushangaza,+ na mtini wangu kuwa kisiki.+ Limeumenya na kuutupilia mbali.+ Matawi yake yamekuwa meupe. 8 Ombolezeni, kama bikira aliyevikwa nguo za magunia+ anavyoomboleza kwa ajili ya mume wa ujana wake.
9 “Toleo la nafaka+ na toleo la kinywaji+ limekatiliwa mbali kutoka katika nyumba ya Yehova; makuhani, walio wahudumu+ wa Yehova, wameomboleza.+ 10 Shamba limeporwa,+ nchi imeomboleza;+ kwa maana nafaka imeporwa, divai mpya imekauka,+ mafuta yamekauka.+ 11 Wakulima wameona aibu;+ watunza-mizabibu wamepiga mayowe, kwa sababu ya ngano na kwa sababu ya shayiri; kwa maana mavuno ya shamba yameangamizwa.+ 12 Mzabibu umekauka, na hata mtini umedhoofika. Nao mkomamanga, pia mtende na mtofaa, miti yote ya shamba imekauka;+ kwa maana furaha imetoweka kwa aibu katika binadamu.+
13 “Jifungeni mshipi, jipigeni vifua,+ ninyi makuhani. Pigeni mayowe, ninyi wahudumu wa madhabahu.+ Ingieni ndani, kaeni usiku kucha mkiwa mmevaa nguo za magunia, ninyi wahudumu wa Mungu wangu; kwa maana nyumba ya Mungu wenu imenyimwa toleo la nafaka+ na toleo la kinywaji.+ 14 Takaseni wakati wa kufunga.+ Iteni kusanyiko kuu.+ Kusanyeni pamoja wanaume wazee, wakaaji wote wa nchi, kwenye nyumba ya Yehova Mungu wenu,+ mlilieni Yehova awape msaada.+
15 “Ole wake siku ile;+ kwa sababu siku ya Yehova iko karibu,+ nayo itakuja kama mporaji kutoka kwa Mweza-Yote! 16 Je, chakula hakijakatiliwa mbali mbele ya macho yetu; kushangilia na furaha kutoka katika nyumba ya Mungu wetu?+ 17 Tini zilizokaushwa zimenyauka chini ya sepetu zake. Maghala yamefanywa ukiwa. Mabanda yamebomolewa, kwa maana nafaka imekauka. 18 Lo! Jinsi mnyama wa kufugwa ameugua! Jinsi makundi ya ng’ombe yamevurugika! Kwa maana hawana malisho.+ Pia, makundi ya kondoo ndiyo yamefanywa yachukue hatia.
19 “Nitakuita wewe, Ee Yehova;+ kwa maana moto umeteketeza malisho ya nyikani, na mwali wa moto umeteketeza miti yote ya mwituni.+ 20 Wanyama wa mwituni pia wanakutamani wewe,+ kwa sababu mifereji ya maji imekauka,+ na moto umeteketeza malisho ya nyikani.”
2 “Pigeni baragumu katika Sayuni,+ pigeni kelele za vita+ katika mlima wangu mtakatifu.+ Wakaaji wote wa nchi na wafadhaike;+ kwa maana siku ya Yehova inakuja,+ kwa maana iko karibu! 2 Siku hiyo ni siku yenye giza na weusi, siku yenye mawingu na weusi mzito,+ kama nuru ya mapambazuko iliyotandazwa juu ya milima.+
“Kuna kundi la watu wengi sana na wenye nguvu;+ kundi kama hilo halijapata kuwako tangu zamani za kale,+ wala baada yake hakutakuwa na lingine tena hata kwa miaka ya kizazi baada ya kizazi. 3 Mbele yake moto umeteketeza,+ na nyuma yake mwali wa moto huteketeza.+ Mbele yake nchi ni kama bustani ya Edeni;+ lakini nyuma yake ni nyika iliyo ukiwa, wala hakuna chochote kinachoponyoka.
4 “Sura yake ni kama sura ya farasi, nao hukimbia kama farasi wa vita.+ 5 Wao hurukaruka kama kwa sauti ya magari juu ya vilele vya milima,+ kama kwa sauti ya mwali wa moto ambao unateketeza majani makavu.+ Wao ni kama kundi la watu wenye nguvu, lililowekwa katika mpangilio wa pigano.+ 6 Vikundi vya watu vitakuwa na maumivu makali kwa sababu yake.+ Nazo nyuso zote zitakuwa na wasiwasi.+
7 “Wanakimbia kama wanaume wenye nguvu.+ Wanapanda ukuta kama wanaume wa vita. Nao huenda kila mmoja katika njia zake, nao hawabadili mapito yao.+ 8 Wala hawasukumani. Wanasonga mbele kama mwanamume katika mwendo wake; na baadhi yao wakianguka katikati ya silaha, wale wengine hawageuzi mwendo wao.
9 “Wao huvuma kuingia jijini. Hukimbia ukutani. Hupanda juu ya nyumba. Wanaingia kupitia madirisha kama mwizi. 10 Mbele yao nchi imefadhaishwa, mbingu zimetikisika. Jua na mwezi zimekuwa na giza,+ na nyota zimeondoa mwangaza wake.+ 11 Naye Yehova atatoa sauti yake+ mbele ya jeshi lake,+ kwa maana kambi yake ina watu wengi sana.+ Kwa maana yeye anayelitimiza neno lake ni mwenye nguvu; maana siku ya Yehova ni kuu+ na yenye kuogopesha sana, naye ni nani anayeweza kustahimili mbele yake?”+
12 “Na sasa pia,” asema Yehova, “rudini kwangu kwa mioyo yenu yote,+ kwa kufunga,+ kwa kulia, na kwa kuomboleza.+ 13 Irarueni mioyo yenu,+ wala si mavazi yenu;+ rudini kwa Yehova Mungu wenu, kwa maana yeye ana neema na rehema,+ si mwepesi wa hasira+ naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo,+ naye hakika atajuta kwa sababu ya msiba huo.+ 14 Ni nani anayejua ikiwa yeye hatageuka na kujuta+ na baada ya hayo abakize baraka,+ toleo la nafaka na toleo la kinywaji kwa ajili ya Yehova Mungu wenu?
15 “Pigeni baragumu katika Sayuni.+ Takaseni wakati wa kufunga.+ Iteni kusanyiko kuu.+ 16 Kusanyeni watu pamoja. Takaseni kutaniko.+ Kusanyeni wazee. Kusanyeni pamoja watoto na wale wanaonyonya.+ Bwana-arusi na atoke katika chumba chake cha ndani, bibi-arusi naye atoke katika chumba chake cha ndoa.
17 “Makuhani, walio wahudumu wa Yehova, na walie kati ya ukumbi na madhabahu,+ wakisema, ‘Ee Yehova, wasikitikie watu wako, usiufanye urithi wako kuwa shutuma,+ mataifa wawatawale. Kwa nini waseme kati ya makabila ya watu: “Yuko wapi Mungu wao?” ’+ 18 Yehova atakuwa mwenye bidii kwa ajili ya nchi yake+ naye atawaonea huruma watu wake.+ 19 Yehova atajibu na kuwaambia watu wake, ‘Tazama nawapelekea ninyi nafaka na divai mpya na mafuta, nanyi mtaishiba;+ nami sitawafanya tena kamwe kuwa shutuma kati ya mataifa.+ 20 Na mkaaji wa kaskazini+ nitamweka mbali kabisa kutoka juu yenu, nami nitamtawanya yeye katika nchi isiyo na maji na iliyo ukiwa, uso wake ukiwa kwenye bahari ya mashariki+ na upande wake wa nyuma kwenye bahari ya magharibi.+ Na uvundo kutoka kwake utapanda, na mnuko kutoka kwake utazidi kupanda;+ kwa maana Yeye atafanya jambo kuu katika yale ambayo Yeye hufanya.’
21 “Usiogope, Ee nchi. Shangilia na ufurahi; kwa maana Yehova atafanya jambo kuu katika yale ambayo Yeye hufanya.+ 22 Msiogope, ninyi wanyama wa mwituni,+ kwa maana malisho ya nyikani yataota majani mabichi.+ Kwa maana mti utatokeza matunda yake.+ Mtini na mzabibu itatokeza nguvu zake.+ 23 Nanyi, wana wa Sayuni, furahini na mshangilie katika Yehova Mungu wenu;+ kwa maana atakuwa na wajibu wa kuwapa mvua ya vuli kwa kiasi kinachofaa,+ naye atawaletea ninyi mvua kubwa, mvua ya vuli na mvua ya masika, kama pale mwanzoni.+ 24 Na viwanja vya kupuria vitajaa nafaka iliyosafishwa, na mitungi ya mashinikizo itafurika kwa divai mpya na mafuta.+ 25 Nami nitawalipa ninyi ridhaa kwa sababu ya miaka ambayo nzige, nzige mchanga, na mende na kiwavi wamekula, jeshi langu kubwa ambalo nimetuma kati yenu.+ 26 Nanyi mtakula, mle na kushiba,+ nanyi mtalisifu jina la Yehova Mungu wenu,+ ambaye amewatendea kwa njia ya ajabu;+ na watu wangu hawataona aibu mpaka wakati usio na kipimo.+ 27 Nanyi mtajua ya kuwa mimi nimo katikati ya Israeli,+ na kwamba mimi ni Yehova Mungu wenu wala hakuna mwingine.+ Na watu wangu hawataona aibu sikuzote.
28 “Kisha itakuwa kwamba nitaimimina roho yangu+ juu ya kila namna ya mwili,+ na wana wenu na binti+ zenu watatoa unabii. Nao wazee wenu wataota ndoto. Nao wanaume wenu vijana wataona maono. 29 Na hata juu ya watumishi wa kiume na juu ya wajakazi katika siku hizo nitaimimina roho yangu.+
30 “Nami nitatoa maajabu mbinguni+ na duniani, damu na moto na nguzo za moshi.+ 31 Jua litageuzwa kuwa giza,+ na mwezi kuwa damu,+ kabla ya kuja kwa ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha.+ 32 Na itakuwa kwamba kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokoka;+ kwa maana katika Mlima Sayuni na katika Yerusalemu kutakuwako wale walioponyoka,+ kama vile ambavyo Yehova amesema, na kati ya waokokaji, ambao Yehova anaita.”+
3 “Kwa maana, tazama! siku hizo na wakati huo,+ nitakapowarudisha mateka wa Yuda na Yerusalemu,+ 2 mimi pia nitayakusanya pamoja mataifa yote+ na kuwaleta kwenye bonde la Yehoshafati;+ nami huko nitajiweka katika hukumu nao kwa sababu ya watu wangu na urithi wangu Israeli,+ ambao wamewatawanya katikati ya mataifa; nao waligawanya nchi yangu mwenyewe.+ 3 Nao waliwapigia kura watu wangu;+ nao walikuwa wakimtoa mtoto wa kiume ili kumpata kahaba,+ walimuuza mtoto wa kike wapate divai ili wanywe.
4 “Pia, mna nini nami, enyi Tiro na Sidoni+ pia nanyi maeneo ya Ufilisti?+ Je, hivyo ndivyo mnavyonitendea kwa kunipa thawabu? Na ikiwa mnanitendea hivyo, matendo yenu nitayalipa haraka, naam, upesi, juu ya vichwa vyenu.+ 5 Kwa sababu ninyi mmechukua fedha yangu mwenyewe na dhahabu yangu,+ nanyi mmeleta vitu vyangu vilivyo vyema katika mahekalu yenu;+ 6 na wana wa Yuda na wana wa Yerusalemu mmewauza+ kwa wana wa Wagiriki,+ kwa kusudi la kuwaondolea mbali kutoka eneo lao wenyewe;+ 7 tazama, ninawaamsha waje kutoka mahali ambapo mmewauza,+ na matendo yenu nitayalipa juu ya vichwa vyenu wenyewe.+ 8 Nami nitawauza wana wenu na binti zenu mikononi mwa wana wa Yuda,+ nao watawauza kwa watu wa Sheba,+ taifa lililo mbali;+ kwa maana Yehova amesema hayo.
9 “Tangazeni mambo haya kati ya mataifa,+ ‘Takaseni vita! Amsheni wanaume wenye nguvu!+ Waacheni wakaribie! Na waje, wanaume wote wa vita!+ 10 Fueni majembe yenu yawe panga na miundu+ yenu iwe mikuki. Aliye dhaifu na aseme: “Mimi ni mwanamume mwenye nguvu.”+ 11 Toeni msaada wenu na mje, enyi mataifa yote jirani,+ mkusanyike pamoja.’ ”+
Mahali pale, Ee Yehova, uwashushe watu wako wenye nguvu.+
12 “Mataifa na yaamshwe, yaje kwenye bonde la Yehoshafati;+ kwa maana hapo nitaketi ili kuhukumu mataifa yote yanayozunguka pande zote.+
13 “Tieni ndani mundu,+ kwa maana mavuno yameiva.+ Njooni, teremkeni, kwa maana shinikizo la divai limejaa.+ Mitungi ya shinikizo inafurika; kwa maana ubaya wao umekuwa mwingi.+ 14 Umati, umati umo katika bonde la uamuzi,+ kwa maana siku ya Yehova iko karibu katika bonde la uamuzi.+ 15 Jua na mwezi vitakuwa giza, na nyota zitaondoa mwangaza wake.+ 16 Na kutoka Sayuni Yehova atanguruma, kutoka Yerusalemu atatoa sauti yake.+ Na mbingu na dunia zitatikisika;+ bali Yehova atakuwa kimbilio kwa watu wake,+ na ngome kwa wana wa Israeli.+ 17 Nanyi mtajua ya kwamba mimi ni Yehova Mungu wenu,+ anayekaa katika Sayuni, mlima wangu mtakatifu.+ Na Yerusalemu litakuwa mahali patakatifu;+ wageni nao hawatapita tena kamwe kati yake.+
18 “Na itakuwa siku hiyo kwamba milima itatiririka divai tamu,+ na vilima vitatiririka maziwa, na sakafu za vijito vya Yuda zitatiririka maji. Na katika nyumba ya Yehova bubujiko litatoka,+ nalo litamwagilia maji bonde la mto la Mishita.+ 19 Nayo Misri itakuwa mahame yenye ukiwa;+ nayo Edomu itakuwa nyika ya mahame yenye ukiwa,+ kwa sababu ya jeuri kwa wana wa Yuda, ambao walimwaga damu isiyo na hatia katika nchi yao.+ 20 Bali Yuda, itakaliwa sikuzote,+ na Yerusalemu kizazi baada ya kizazi.+ 21 Na damu yao ambayo niliiona kuwa ina hatia nitaiona kuwa haina hatia;+ Yehova naye atakuwa anakaa katika Sayuni.”+