Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt Zekaria 1:1-14:21
  • Zekaria

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Zekaria
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Zekaria

ZEKARIA

1 Katika mwezi wa nane, mwaka wa pili wa utawala wa Dario,+ neno la Yehova lilimjia nabii Zekaria*+ mwana wa Berekia mwana wa Ido, likisema: 2 “Yehova aliwakasirikia vikali baba zenu.+

3 “Waambie, ‘Yehova wa majeshi anasema hivi: “‘Nirudieni,’ asema Yehova wa majeshi, ‘nami nitawarudia ninyi,’+ asema Yehova wa majeshi.”’

4 “‘Msiwe kama baba zenu walioambiwa hivi na manabii wa kale: “Yehova wa majeshi anasema, ‘Tafadhali, geukeni* kutoka katika njia zenu ovu na matendo yenu maovu.’”’+

“‘Lakini hawakusikiliza, wala hawakunikazia uangalifu,’+ asema Yehova.

5 “‘Baba zenu wako wapi sasa? Na je, manabii wanaishi milele? 6 Hata hivyo, je, maneno yangu na maagizo yangu niliyowaamuru watumishi wangu, manabii, hayakutimia kwa baba zenu?’+ Basi wakanirudia na kusema: ‘Yehova wa majeshi ametutendea kulingana na njia zetu na matendo yetu, kama alivyokusudia kututendea.’”+

7 Katika siku ya 24 ya mwezi wa 11, yaani, mwezi wa Shebati,* katika mwaka wa pili wa utawala wa Dario,+ neno la Yehova lilimjia nabii Zekaria mwana wa Berekia mwana wa Ido, likisema: 8 “Niliona maono wakati wa usiku. Nilimwona mtu akiendesha farasi mwekundu, akasimama tuli bondeni katikati ya miti ya mihadasi; na nyuma yake kulikuwa na farasi wekundu, wa kahawia, na weupe.”

9 Basi nikauliza: “Hawa ni nani, bwana wangu?”

Malaika aliyekuwa akizungumza nami akanijibu: “Nitakuonyesha hawa ni nani.”

10 Kisha mtu huyo aliyesimama tuli katikati ya mihadasi akasema: “Hawa ndio wale ambao Yehova amewatuma watembee huku na huku duniani.” 11 Nao wakamwambia malaika huyo wa Yehova aliyekuwa amesimama katikati ya mihadasi: “Tumetembea huku na huku duniani, na tazama! dunia yote imetulia na haina vurugu.”+

12 Basi malaika wa Yehova akauliza: “Ee Yehova wa majeshi, utaendelea hadi lini kukataa kuwaonyesha rehema wakaaji wa Yerusalemu na wa majiji ya Yuda,+ ambao umewakasirikia kwa miaka hii 70?”+

13 Yehova akamjibu kwa maneno ya fadhili na yenye kufariji malaika huyo aliyekuwa akizungumza nami. 14 Kisha malaika huyo aliyekuwa akizungumza nami akaniambia: “Tangaza hivi kwa sauti, ‘Yehova wa majeshi anasema hivi: “Nina bidii kwa ajili ya Yerusalemu na Sayuni, bidii nyingi.+ 15 Kwa hasira kali nimeyakasirikia mataifa yanayostarehe,+ kwa sababu niliwakasirikia kidogo watu wangu,+ lakini yalizidisha msiba wao.”’+

16 “Basi Yehova anasema hivi: ‘“Nitarudi Yerusalemu kwa rehema,+ na nyumba yangu mwenyewe itajengwa humo,”+ asema Yehova wa majeshi, “na kamba ya kupimia itanyooshwa juu ya Yerusalemu.”’+

17 “Tangaza tena hivi kwa sauti: ‘Yehova wa majeshi anasema, “Majiji yangu yatafurika wema tena; na Yehova atalifariji tena Sayuni+ na kulichagua tena Yerusalemu.”’”+

18 Kisha nikatazama juu na kuona pembe nne.+ 19 Kwa hiyo nikamuuliza malaika aliyekuwa akizungumza nami: “Pembe hizi zinamaanisha nini?” Akanijibu: “Pembe hizi ndizo zilizowatawanya watu wa Yuda,+ Israeli,+ na Yerusalemu.”+

20 Kisha Yehova akanionyesha mafundi wanne. 21 Nikauliza: “Hawa wanakuja kufanya nini?”

Akajibu: “Hizi ndizo pembe zilizowatawanya watu wa Yuda hivi kwamba hakuna yeyote aliyeweza kuinua kichwa chake. Mafundi hawa watakuja kuzitisha, kuziangusha chini pembe za mataifa yaliyoinua pembe zao dhidi ya nchi ya Yuda, ili kuwatawanya wakaaji wake.”

2 Nami nikatazama juu na kumwona mtu akiwa na kamba ya kupimia+ mkononi mwake. 2 Kwa hiyo nikamuuliza: “Unaenda wapi?”

Akanijibu: “Naenda kupima jiji la Yerusalemu, ili nijue upana wake na urefu wake.”+

3 Na tazama! malaika aliyekuwa akizungumza nami akaondoka, na malaika mwingine akaja kukutana naye. 4 Kisha akamwambia: “Kimbia ukamwambie yule kijana, ‘“Yerusalemu litakaliwa+ kama eneo la mashambani lililo wazi,* kwa sababu ya watu wengi na mifugo mingi iliyomo.+ 5 Nitakuwa ukuta wa moto kulizunguka pande zote,”+ asema Yehova, “nami nitakuwa utukufu ndani yake.”’”+

6 “Njooni! Njooni! Kimbieni kutoka nchi ya kaskazini,”+ asema Yehova.

“Kwa maana nimewatawanya kuelekea pepo nne za mbinguni,”*+ asema Yehova.

7 “Njoo, Ee Sayuni! Kimbia, wewe unayekaa na binti ya Babiloni.+ 8 Kwa maana hivi ndivyo anavyosema Yehova wa majeshi, ambaye baada ya kutukuzwa* amenituma kwa mataifa yaliyokuwa yakiwapora ninyi:+ ‘Yeyote anayewagusa ninyi anaigusa mboni ya jicho langu.*+ 9 Kwa maana sasa nitaupunga mkono wangu dhidi yao, nao watakuwa nyara kwa watumwa wao wenyewe.’+ Na hakika mtajua kwamba Yehova wa majeshi amenituma.

10 “Paza sauti kwa shangwe, Ee binti ya Sayuni;+ kwa maana ninakuja,+ nami nitakaa kati yako,”+ asema Yehova. 11 “Mataifa mengi yatajiunga na Yehova siku hiyo,+ nao watakuwa watu wangu; nami nitakaa kati yenu.” Nanyi mtalazimika kujua kwamba Yehova wa majeshi amenituma kwenu. 12 Yehova atamiliki Yuda kama fungu lake katika ardhi takatifu, naye atalichagua tena jiji la Yerusalemu.+ 13 Nyamazeni, enyi nyote wenye mwili,* mbele za Yehova, kwa maana anachukua hatua kutoka katika makao yake matakatifu.

3 Naye akanionyesha kuhani mkuu Yoshua+ akiwa amesimama mbele ya malaika wa Yehova, na Shetani+ alikuwa amesimama kwenye mkono wa kulia wa Yoshua ili kumpinga. 2 Kisha malaika wa Yehova akamwambia Shetani: “Yehova na akukemee, ewe Shetani,+ naam, Yehova, ambaye amechagua Yerusalemu,+ na akukemee! Je, mtu huyu si gogo lililochomolewa motoni?”

3 Sasa Yoshua alikuwa amevaa mavazi machafu akiwa amesimama mbele ya malaika. 4 Malaika akawaambia wale waliokuwa wamesimama mbele yake, “Mvueni mavazi yake machafu.” Kisha akamwambia Yoshua, “Tazama! Nimefuta kosa lako,* nawe utavishwa mavazi bora.”*+

5 Basi nikasema: “Na avikwe kilemba safi kichwani.”+ Nao wakamvika kilemba safi kichwani na kumvisha mavazi; na malaika wa Yehova alikuwa amesimama karibu. 6 Kisha malaika wa Yehova akamwambia Yoshua: 7 “Yehova wa majeshi anasema hivi, ‘Ikiwa utatembea katika njia zangu na kutekeleza majukumu niliyokupa, utakuwa mwamuzi nyumbani mwangu+ na kuzitunza* nyua zangu; nami nitakuruhusu ufike mbele zangu, pamoja na hawa wanaosimama hapa.’

8 “‘Tafadhali sikiliza, Ee Kuhani Mkuu Yoshua, wewe pamoja na wenzako wanaoketi mbele yako, kwa maana wanaume hawa ni ishara; tazama! ninamleta mtumishi wangu+ anayeitwa Chipukizi!+ 9 Tazama jiwe ambalo nimeweka mbele ya Yoshua! Jiwe hili moja lina macho saba; nami ninachonga maandishi juu yake,’ asema Yehova wa majeshi, ‘nami nitaondoa hatia ya nchi hiyo kwa siku moja.’+

10 “‘Siku hiyo,’ asema Yehova wa majeshi, ‘kila mmoja wenu atamwalika jirani yake aje chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake.’”+

4 Malaika aliyekuwa akizungumza nami akarudi na kuniamsha, kama mtu anavyoamshwa kutoka usingizini. 2 Kisha akaniuliza: “Unaona nini?”

Nikamjibu: “Tazama! ninaona kinara cha taa cha dhahabu tupu,+ na juu yake kuna bakuli. Kina taa saba juu yake,+ naam, saba, na taa hizo zilizo juu yake zina mirija saba. 3 Na kando yake kuna mizeituni miwili,+ mmoja upande wa kulia wa bakuli na mwingine upande wa kushoto.”

4 Kisha nikamuuliza malaika aliyekuwa akizungumza nami: “Bwana wangu, vitu hivi vinamaanisha nini?” 5 Kwa hiyo malaika aliyekuwa akizungumza nami akaniuliza: “Hujui maana ya vitu hivi?”

Nikamjibu: “Sijui, bwana wangu.”

6 Ndipo akaniambia: “Hili ndilo neno la Yehova kwa Zerubabeli: ‘“Si kwa jeshi, wala si kwa nguvu,+ bali kwa roho yangu,”+ asema Yehova wa majeshi. 7 Wewe ni nani, Ee mlima mkubwa? Mbele ya Zerubabeli+ utakuwa nchi tambarare.*+ Naye ataleta nje jiwe la juu kabisa la hekalu huku watu wakishangilia: “Ni zuri ajabu! Ni zuri ajabu!”’”

8 Neno la Yehova likanijia tena, likisema: 9 “Mikono ya Zerubabeli imeweka msingi wa nyumba hii,+ na mikono yake mwenyewe itaikamilisha.+ Nanyi mtalazimika kujua kwamba Yehova wa majeshi amenituma kwenu. 10 Kwa maana ni nani ameidharau siku inayoanza kwa mambo madogo?*+ Kwa maana watashangilia na kuona timazi* mkononi mwa Zerubabeli. Na haya macho saba ni macho ya Yehova, ambayo yanazunguka duniani kote.”+

11 Kisha nikamuuliza: “Mizeituni hii miwili iliyo upande wa kulia na wa kushoto wa kinara cha taa inamaanisha nini?”+ 12 Nikamuuliza mara ya pili: “Mafungu haya mawili ya matawi ya mizeituni* yanayomimina mafuta ya dhahabu kupitia mirija miwili ya dhahabu yanamaanisha nini?”

13 Basi akaniuliza: “Hujui maana ya vitu hivi?”

Nikamjibu: “Sijui, bwana wangu.”

14 Akasema: “Hawa ndio wale watiwa-mafuta wawili wanaosimama kando ya Bwana wa dunia yote.”+

5 Nikatazama juu tena, nikaona kitabu cha kukunjwa kikipaa. 2 Akaniuliza: “Unaona nini?”

Nikamjibu: “Ninaona kitabu cha kukunjwa chenye urefu wa mikono 20* na upana wa mikono 10 kikipaa.”

3 Kisha akaniambia: “Hii ndiyo laana inayotoka kwenda juu ya dunia yote, kwa sababu kila mtu anayeiba,+ kama ilivyoandikwa upande mmoja, hajaadhibiwa; na kila mtu anayeapa kwa uwongo,+ kama ilivyoandikwa upande wa pili, hajaadhibiwa. 4 ‘Nimeituma laana hiyo,’ asema Yehova wa majeshi, ‘nayo itaingia katika nyumba ya mwizi na katika nyumba ya mtu anayeapa kwa uwongo katika jina langu; nayo itakaa katika nyumba hiyo na kuiharibu kabisa na pia mbao zake na mawe yake.’”

5 Ndipo malaika aliyekuwa akizungumza nami akaja na kuniambia: “Tafadhali, tazama juu, uone kitu kinachotoka.”

6 Kwa hiyo nikamuuliza: “Ni kitu gani hicho?”

Akanijibu: “Ni chombo cha efa kinachotoka.”* Kisha akaniambia: “Hivyo ndivyo wanavyoonekana duniani kote.” 7 Nami nikaona kwamba kifuniko chake cha mviringo cha madini ya risasi kilikuwa kimeinuliwa, na kulikuwa na mwanamke aliyekuwa ameketi ndani ya chombo hicho. 8 Kwa hiyo malaika akasema: “Huu ni Uovu.” Kisha akamsukuma mwanamke huyo ndani ya chombo hicho cha efa na kukifunika kwa nguvu kwa kile kifuniko kizito cha madini ya risasi.

9 Halafu nikatazama juu na kuwaona wanawake wawili wakija, nao walikuwa wakipaa katika upepo. Walikuwa na mabawa kama ya korongo. Nao wakakiinua kile chombo na kuruka nacho kati ya dunia na mbingu. 10 Basi nikamuuliza malaika aliyekuwa akizungumza nami: “Wanakipeleka wapi chombo cha efa?”

11 Akanijibu: “Katika nchi ya Shinari*+ ili wamjengee nyumba mwanamke huyo; na itakapokuwa tayari, atawekwa humo mahali panapomfaa.”

6 Kisha nikatazama juu tena na kuona magari manne ya vita yakitoka katikati ya milima miwili, na milima hiyo ilikuwa ya shaba. 2 Gari la kwanza lilikokotwa na farasi wekundu, na gari la pili, farasi weusi.+ 3 Gari la tatu lilikokotwa na farasi weupe, na gari la nne, farasi wenye madoadoa na mabaka.+

4 Nikamuuliza malaika aliyekuwa akizungumza nami: “Magari haya yanamaanisha nini bwana wangu?”

5 Malaika huyo akanijibu: “Hizi ni zile roho nne+ za mbinguni zinazotoka baada ya kusimama mbele ya Bwana wa dunia yote.+ 6 Gari linalokokotwa na farasi weusi linaenda katika nchi ya kaskazini;+ farasi weupe wanaenda kuvuka bahari; na wale wenye madoadoa wanaenda katika nchi ya kusini. 7 Na farasi wenye mabaka walitamani sana kwenda kutembea kotekote duniani.” Kisha akasema: “Nendeni, tembeeni kotekote duniani.” Nao wakaanza kutembea kotekote duniani.

8 Kisha akaniita kwa sauti na kuniambia: “Tazama, farasi wanaoenda katika nchi ya kaskazini wameifanya roho ya Yehova itulie katika nchi ya kaskazini.”

9 Neno la Yehova likanijia tena, likisema: 10 “Chukua vitu ambavyo Heldai, Tobaya, na Yedaya walileta kutoka kwa watu walio uhamishoni; na siku hiyo, ni lazima uende katika nyumba ya Yosia mwana wa Sefania ukiwa pamoja na watu hawa waliotoka Babiloni. 11 Unapaswa kuchukua fedha na dhahabu, utengeneze taji* na kumvika kichwani Yoshua+ mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu. 12 Nawe umwambie,

“‘Yehova wa majeshi anasema hivi: “Ndiye huyu mwanamume anayeitwa Chipukizi.+ Atachipuka kutoka mahali pake mwenyewe, naye atalijenga hekalu la Yehova.+ 13 Yeye ndiye atakayelijenga hekalu la Yehova, na ndiye atakayepokea utukufu. Ataketi kwenye kiti chake cha ufalme na kutawala, naye atakuwa pia kuhani kwenye kiti chake cha ufalme,+ na kutakuwa na mapatano ya amani kati ya hivyo viwili.* 14 Na taji hilo* litakuwa kumbukumbu* kwa Helemu, Tobaya, Yedaya,+ na Heni mwana wa Sefania, katika hekalu la Yehova. 15 Na wale walio mbali sana watakuja na kushiriki katika ujenzi wa hekalu la Yehova.” Nanyi mtalazimika kujua kwamba Yehova wa majeshi amenituma kwenu. Na itakuwa hivyo—ikiwa hamtakosa kuisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu.’”

7 Na katika mwaka wa nne wa utawala wa Mfalme Dario, neno la Yehova lilimjia Zekaria+ siku ya nne ya mwezi wa tisa, yaani, mwezi wa Kislevu.* 2 Watu wa Betheli walimtuma Shareza na Regem-meleki na wanaume wake ili wamwombe Yehova kibali,* 3 wawaulize hivi makuhani wa nyumba ya* Yehova wa majeshi na pia manabii: “Je, nilie katika mwezi wa tano+ na kujinyima chakula, kama vile ambavyo nimekuwa nikifanya kwa miaka mingi sana?”

4 Neno la Yehova wa majeshi likanijia tena, likisema: 5 “Waambie watu wote nchini na makuhani, ‘Mlipofunga na kulia kwa sauti katika mwezi wa tano na mwezi wa saba+ kwa miaka 70,+ je, kweli mlifunga kwa ajili yangu? 6 Na mlipokuwa mkila na kunywa, je, hamkuwa mkila na kunywa kwa ajili yenu wenyewe? 7 Je, hampaswi kutii maneno ambayo Yehova alitangaza kupitia manabii wa kale,+ wakati jiji la Yerusalemu na majiji yaliyolizunguka yalipokuwa na wakaaji na yalipokuwa na amani, na watu walipokaa Negebu na Shefela?’”

8 Neno la Yehova likamjia tena Zekaria, likisema: 9 “Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Hukumuni kwa haki ya kweli,+ na mtendeane kwa upendo mshikamanifu+ na rehema. 10 Msimpunje mjane wala yatima,*+ mgeni+ wala maskini;+ na katika mioyo yenu msipangiane njama za kutendeana uovu.’+ 11 Lakini waliendelea kukataa kusikiliza,+ wakageuza migongo yao kwa ukaidi,+ na kuziba masikio yao ili wasisikie.+ 12 Waliifanya mioyo yao iwe kama almasi*+ nao walikataa kutii sheria* na maneno ambayo Yehova wa majeshi aliwapa kwa roho yake kupitia manabii wa kale.+ Kwa hiyo Yehova wa majeshi akakasirika sana.”+

13 “‘Kama vile ambavyo hawakunisikiliza nilipowaita,+ mimi pia sikuwasikiliza waliponiita,’+ asema Yehova wa majeshi. 14 ‘Nami niliwatawanya kwa kimbunga kotekote katika mataifa yote ambayo hawakuyajua,+ na nchi ikaachwa ukiwa nyuma yao, hivi kwamba hakuna yeyote aliyeingia wala kutoka;+ kwa maana waliibadili nchi yenye kutamanika ikawa kitu cha kutisha.’”

8 Neno la Yehova wa majeshi lilinijia tena, likisema: 2 “Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Nitakuwa na bidii kwa ajili ya Sayuni, bidii nyingi,+ na kwa hasira kali nitakuwa na bidii kwa ajili yake.’”

3 “Yehova anasema hivi: ‘Nitarudi Sayuni+ na kukaa Yerusalemu;+ na Yerusalemu litaitwa jiji la ukweli,*+ na mlima wa Yehova wa majeshi utaitwa mlima mtakatifu.’”+

4 “Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Wanaume wazee na wanawake wazee wataketi tena katika viwanja vya jiji la Yerusalemu, kila mmoja wao akiwa na mkongojo wake mkononi kwa sababu ya umri wake mkubwa.*+ 5 Na viwanja vya jiji vitajaa wavulana na wasichana wanaocheza.’”+

6 “Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Ingawa jambo hilo huenda likaonekana kuwa gumu kwa watu wa taifa hili watakaobaki siku hizo, je, linaweza kuwa gumu sana machoni pangu pia?’ asema Yehova wa majeshi.”

7 “Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Tazama, ninawaokoa watu wangu kutoka katika nchi ya mashariki na nchi ya magharibi.*+ 8 Nami nitawaleta ndani, nao wataishi Yerusalemu;+ watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao+ katika ukweli* na katika uadilifu.’”

9 “Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Mikono yenu na iwe na nguvu,*+ ninyi ambao sasa mnasikia maneno haya yanayotoka katika kinywa cha manabii,+ maneno yaleyale yaliyosemwa siku ambayo msingi wa nyumba ya Yehova wa majeshi uliwekwa ili hekalu lijengwe. 10 Kwa maana kabla ya wakati huo, mshahara haukulipwa kwa ajili ya mwanadamu wala kwa ajili ya mnyama;+ na haikuwa salama kuingia wala kutoka kwa sababu ya maadui, kwa maana nilisababisha uadui kati ya watu wote.’

11 “‘Lakini sasa sitawatendea watu waliobaki wa taifa hili kama nilivyowatendea zamani,’+ asema Yehova wa majeshi. 12 ‘Kwa maana mbegu ya amani itapandwa; mzabibu utazaa matunda yake na dunia itatoa mazao yake,+ na mbingu zitatoa umande wake; nami nitawapa watu waliobaki wa taifa hili vitu hivi vyote viwe urithi wao.+ 13 Na kama mlivyokuwa kitu cha kulaaniwa miongoni mwa mataifa,+ Ee nyumba ya Yuda na nyumba ya Israeli, vivyo hivyo nitawaokoa, nanyi mtakuwa baraka.+ Msiogope!+ Mikono yenu na iwe na nguvu.’*+

14 “Kwa maana Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘“Kama nilivyokusudia kuwaletea msiba kwa sababu mababu zenu walinikasirisha,” asema Yehova wa majeshi, “nami sikughairi,+ 15 ndivyo nilivyokusudia sasa kulitendea mema jiji la Yerusalemu na nyumba ya Yuda.+ Msiogope!”’+

16 “‘Haya ndiyo mambo mnayopaswa kufanya: Kila mtu amwambie mwenzake ukweli,+ na hukumu mnazotoa katika malango yenu zinapaswa kutetea ukweli na amani.+ 17 Msipangiane njama za msiba mioyoni mwenu,+ nanyi msipende kiapo chochote cha uwongo;+ kwa maana hayo yote ni mambo ninayochukia,’+ asema Yehova.”

18 Neno la Yehova wa majeshi lilinijia tena, likisema: 19 Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Mfungo wa mwezi wa nne,+ mfungo wa mwezi wa tano,+ mfungo wa mwezi wa saba,+ na mfungo wa mwezi wa kumi+ zitakuwa pindi za shangwe na kushangilia kwa ajili ya nyumba ya Yuda—sherehe za kushangilia.+ Kwa hiyo pendeni ukweli na amani.’

20 “Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Itatukia kwamba mataifa na wakaaji wa majiji mengi watakuja; 21 na wakaaji wa jiji moja wataenda kwa wakaaji wa jiji lingine na kuwaambia: “Twendeni kwa bidii tukamsihi Yehova atupe kibali chake* na kumtafuta Yehova wa majeshi. Mimi pia nitaenda.”+ 22 Na mataifa mengi na mataifa yenye nguvu yatakuja Yerusalemu kumtafuta Yehova wa majeshi + na kumsihi Yehova awape kibali chake.’*

23 “Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Siku hizo watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa+ watashika, naam, watashika kwa nguvu joho* la Myahudi,* wakisema: “Tunataka kwenda pamoja nanyi,+ kwa maana tumesikia kwamba Mungu yupo pamoja nanyi.”’”+

9 Tangazo:

“Neno la Yehova liko dhidi ya nchi ya Hadraki,

Nalo linalenga* Damasko+

—Kwa maana macho ya Yehova yanawaangalia wanadamu+

Na makabila yote ya Israeli—

 2 Na dhidi ya Hamathi,+ inayopakana nayo,

Na dhidi ya majiji ya Tiro+ na Sidoni,+ kwa maana yana hekima nyingi.+

 3 Jiji la Tiro lilijijengea boma.*

Lilirundika fedha kama mavumbi

Na dhahabu kama mavumbi barabarani.+

 4 Tazama! Yehova atachukua mali za jiji hilo,

Naye ataliangamiza jeshi lake baharini;+

Na jiji hilo litateketezwa motoni.+

 5 Jiji la Ashkeloni litaona jambo hilo na kuogopa;

Gaza litahisi maumivu makali sana,

Ekroni pia, kwa sababu tumaini lake limeaibishwa.

Mfalme wa Gaza ataangamizwa,

Na Ashkeloni halitakaliwa na watu.+

 6 Mwanaharamu ataishi Ashdodi,

Nami nitakikomesha kiburi cha Mfilisti.+

 7 Nitaondoa vitu vyenye damu kutoka kinywani mwake

Na vitu vyenye kuchukiza kutoka katikati ya meno yake,

Naye atabaki kwa ajili ya Mungu wetu;

Naye atakuwa kama shehe* nchini Yuda,+

Na Ekroni kama Myebusi.+

 8 Nitapiga kambi nikiwa mlinzi wa nyumba yangu,+

Hivi kwamba hakuna yeyote atakayeingia na hakuna yeyote atakayetoka;

Na hakuna msimamizi wa watumwa* atakayeingia humo tena,+

Kwa maana sasa nimeyaona* kwa macho yangu.

 9 Shangilia sana, Ee binti ya Sayuni.

Paza sauti kwa ushindi, Ee binti ya Yerusalemu.

Tazama! Mfalme wako anakuja kwako.+

Yeye ni mwadilifu, analeta wokovu,*

Ni mnyenyekevu+ na amepanda punda,

Amepanda mwanapunda dume,* mwana wa punda jike.+

10 Nitaondoa gari la vita Efraimu

Na farasi kutoka Yerusalemu.

Upinde wa vita utachukuliwa.

Naye atatangaza amani kwa mataifa;+

Utawala wake utaenea kutoka bahari mpaka bahari

Na kutoka Mto Efrati mpaka kwenye miisho ya dunia.+

11 Lakini wewe, Ee mwanamke, kwa damu ya agano lako,

Nitawatoa wafungwa wako katika shimo lisilo na maji.+

12 Rudini katika ngome, enyi wafungwa wenye tumaini.+

Leo ninakwambia,

‘Nitakulipa fungu maradufu, ewe mwanamke.+

13 Kwa maana nitampinda* Yuda kama upinde wangu.

Nitamjaza Efraimu kwenye upinde,*

Nami nitawaamsha wana wako, Ee Sayuni,

Dhidi ya wana wako, Ee Ugiriki,

Nami nitakufanya uwe kama upanga wa shujaa.’

14 Itaonekana kwamba Yehova yupo pamoja nao,

Na mshale wake utafyatuka kama radi.

Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova atapiga pembe,+

Naye atasonga mbele pamoja na dhoruba za upepo za kusini.

15 Yehova wa majeshi atawalinda,

Nao watayameza na kuyatiisha mawe ya kombeo.+

Watakunywa na kupiga kelele, kana kwamba wamekunywa divai;

Nao watajazwa kama bakuli,

Kama pembe za madhabahu.+

16 Yehova Mungu wao atawaokoa siku hiyo

Wakiwa kundi la watu wake;+

Kwa maana watakuwa kama vito vya taji vinavyong’aa kwenye ardhi yake.+

17 Jinsi wema wake ulivyo mwingi kwelikweli,+

Na jinsi uzuri wake unavyovutia ajabu!

Nafaka itawafanya vijana wanaume wanawiri,

Na divai mpya itawafanya mabikira wanawiri.”+

10 “Mwombeni Yehova mvua wakati wa mvua ya masika.

Yehova ndiye anayetengeneza mawingu ya dhoruba,

Ndiye anayewaletea mvua,+

Na kumpa kila mtu mimea ya shambani.

 2 Kwa maana sanamu za terafimu* zimesema uwongo;*

Na wabashiri* wameona maono ya uwongo.

Husimulia ndoto zisizo na faida,

Na kwa ubatili wao hujaribu kufariji.

Ndiyo sababu watatangatanga kama kondoo.

Watateseka, kwa maana hakuna mchungaji.

 3 Hasira yangu inawaka dhidi ya wachungaji,

Nitawaadhibu viongozi* wanaowakandamiza watu;

Kwa maana Yehova wa majeshi amelielekezea uangalifu kundi lake,+ ameielekezea uangalifu nyumba ya Yuda,

Naye amewafanya wawe kama farasi wake mwenye fahari vitani.

 4 Mtu mkuu anatoka kwake,*

Mtawala anayemtegemeza anatoka kwake,*

Upinde wa vita unatoka kwake;

Na kila mwangalizi* hutoka kwake, wote pamoja.

 5 Nao watakuwa kama mashujaa,

Wanaokanyaga matope barabarani wakiwa vitani.

Watapigana vita, kwa maana Yehova yupo pamoja nao;+

Na wapanda farasi wataaibishwa.+

 6 Nitaifanya nyumba ya Yuda iwe kuu sana,

Nami nitaiokoa nyumba ya Yosefu.+

Nitawarudisha,

Kwa maana nitawaonyesha rehema;+

Nao watakuwa kama watu ambao sijawahi kuwatupa;+

Kwa maana mimi ni Yehova Mungu wao, nami nitawajibu.

 7 Ni lazima watu wa Efraimu wawe kama shujaa hodari,

Na moyo wao utashangilia kana kwamba wamekunywa divai.+

Wana wao wataona jambo hilo na kushangilia;

Moyo wao utashangilia katika Yehova.+

 8 ‘Nitawapigia mluzi na kuwakusanya pamoja;

Kwa maana nitawakomboa,+ nao watakuwa wengi,

Na kuendelea kuongezeka.

 9 Ingawa ninawatawanya kama mbegu miongoni mwa mataifa,

Watanikumbuka wakiwa katika maeneo ya mbali;

Watahuishwa na kurudi pamoja na wana wao.

10 Nitawarudisha kutoka nchini Misri

Na kuwakusanya kutoka Ashuru;+

Nitawaleta katika nchi ya Gileadi+ na Lebanoni,

Na hakutakuwa na nafasi zaidi ya kuwatosha.+

11 Ni lazima apite baharini kwa msukosuko;

Na humo baharini atayapiga mawimbi yatulie;+

Vilindi vyote vya Mto Nile vitakauka.

Kiburi cha Ashuru kitashushwa,

Na fimbo ya mfalme wa Misri itaondoka.+

12 Nitawafanya wawe wakuu sana katika jina langu Yehova,+

Nao watatembea huku na kule katika jina langu,’+ asema Yehova.”

11 “Fungua milango yako, Ee Lebanoni,

Ili moto uteketeze mierezi yako.

 2 Omboleza kwa sauti, ewe mberoshi, kwa maana mwerezi umeanguka;

Miti mikubwa imeharibiwa!

Ombolezeni kwa sauti, enyi mialoni ya Bashani,

Kwa maana msitu mnene umefyekwa!

 3 Sikilizeni! Maombolezo ya wachungaji,

Kwa maana fahari yao imeharibiwa.

Sikilizeni! Mingurumo ya wanasimba,*

Kwa maana mapori makubwa yaliyo kwenye kingo za Yordani yameharibiwa.

4 “Yehova Mungu wangu anasema hivi: ‘Lichunge kundi la kondoo wanaopaswa kuchinjwa,+ 5 ambao wanachinjwa na wanunuzi wao+ lakini wanunuzi hao hawahesabiwi kuwa na hatia. Na wale wanaowauza+ husema, “Yehova na asifiwe, kwa maana nitakuwa tajiri.” Na wachungaji wao hawawahurumii.’+

6 “‘Kwa maana sitawahurumia tena wakaaji wa nchi,’ asema Yehova. ‘Kwa hiyo nitamtia kila mtu mikononi mwa jirani yake na mfalme wake; nao wataipondaponda nchi, nami sitawaokoa kutoka mikononi mwao.’”

7 Nami nikaanza kulichunga kundi la kondoo wanaopaswa kuchinjwa,+ kwa faida yenu, enyi kondoo mnaoteseka. Kwa hiyo nikachukua fimbo mbili, moja nikaiita Uzuri, na nyingine Muungano,+ nikaanza kulichunga kundi hilo la kondoo.⁠ 8 Nami nikawafukuza wachungaji watatu katika mwezi mmoja, kwa maana nilichoshwa nao, nao pia wakachukizwa nami. 9 Kisha nikasema: “Sitaendelea kuwachunga ninyi. Yule anayekufa na afe, na yule anayeangamia na aangamie. Na wale wanaobaki, kila mmoja wao amle mwenzake.” 10 Basi nikachukua fimbo yangu inayoitwa Uzuri+ na kuikatakata, na hivyo nikavunja agano langu nililokuwa nimefanya na mataifa yote. 11 Basi likavunjika siku hiyo, na kondoo walioteseka waliokuwa wakinitazama walijua kwamba hilo lilikuwa neno la Yehova.

12 Kisha nikawaambia: “Ikiwa mnaona ni vema, nipeni mshahara wangu; kama sivyo, msinipe.” Basi wakanilipa* mshahara wangu, vipande 30 vya fedha.+

13 Ndipo Yehova akaniambia: “Vitupe katika hazina—thamani kubwa waliyonikadiria.”+ Kwa hiyo nikavichukua vipande hivyo 30 vya fedha na kuvitupa katika hazina ya nyumba ya Yehova.+

14 Kisha nikaikatakata fimbo yangu ya pili, inayoitwa Muungano,+ na hivyo nikauvunja undugu kati ya Yuda na Israeli.+

15 Na Yehova akaniambia: “Sasa vichukue vifaa vya mchungaji asiyefaa.+ 16 Kwa maana ninamruhusu mchungaji ainuke nchini. Hatawatunza kondoo wanaoangamia;+ hatawatafuta walio wachanga au kuwaponya waliojeruhiwa+ au kuwalisha wanaoweza kusimama. Badala yake, atamla kondoo aliyenona+ na kuwang’oa kwato kondoo.+

17 Ole wake mchungaji wangu asiyefaa,+ anayeliacha kundi!+

Upanga utakata mkono wake na jicho lake la kulia.

Mkono wake utapooza kabisa,

Na jicho lake la kulia litapofuka* kabisa.”

12 Tangazo:

“Neno la Yehova kuhusu Israeli,” asema Yehova,

Yule aliyezitandaza mbingu,+

Aliyeweka msingi wa dunia,+

Na kuumba roho* iliyo ndani ya mwanadamu.

2 “Tazama, ninafanya jiji la Yerusalemu liwe kikombe kinachosababisha* mataifa yote jirani yapepesuke; na jiji la Yuda litazingirwa, na pia Yerusalemu.+ 3 Siku hiyo nitafanya Yerusalemu liwe jiwe zito* kwa mataifa yote. Kwa hakika wote watakaolinyanyua watajeruhiwa vibaya;+ na mataifa yote duniani yatakusanyika kupigana na jiji hilo.+ 4 Siku hiyo,” asema Yehova, “nitamtia hofu kila farasi na kumtia wazimu yule anayempanda. Nitaikazia macho nyumba ya Yuda, lakini nitampofusha kila farasi wa mataifa. 5 Na mashehe* wa Yuda watasema moyoni mwao, ‘Wakaaji wa Yerusalemu ni nguvu kwetu kwa sababu ya Yehova wa majeshi Mungu wao.’+ 6 Siku hiyo nitawafanya mashehe wa Yuda wawe kama chungu cha moto kati ya kuni na kama mwenge unaowaka kati ya safu ya miganda iliyokatwa ya nafaka,+ nao watayateketeza mataifa yote jirani yaliyo upande wa kulia na wa kushoto;+ na jiji la Yerusalemu litakuwa tena na wakaaji mahali pake,* huko Yerusalemu.+

7 “Na Yehova atayaokoa kwanza mahema ya Yuda, ili umaridadi wa* nyumba ya Daudi na umaridadi wa* wakaaji wa Yerusalemu usizidi sana ule wa Yuda. 8 Siku hiyo Yehova atakuwa ulinzi kuwazunguka wakaaji wa Yerusalemu;+ siku hiyo yule anayejikwaa* kati yao atakuwa kama Daudi, na nyumba ya Daudi itakuwa kama Mungu, kama malaika wa Yehova anayetangulia mbele yao.+ 9 Na siku hiyo, kwa hakika nitayaangamiza mataifa yote yatakayokuja kushambulia Yerusalemu.+

10 “Nitamimina roho ya kibali na dua juu ya nyumba ya Daudi na juu ya wakaaji wa Yerusalemu, nao watamtazama yule waliyemchoma,+ watamwombolezea kwa sauti kama ambavyo wangemwombolezea mwana wa pekee; watamhuzunikia sana kama ambavyo wangemhuzunikia mwana mzaliwa wa kwanza. 11 Siku hiyo kutakuwa na maombolezo makubwa Yerusalemu, kama maombolezo ya Hadadrimoni katika Nchi Tambarare ya Megido.+ 12 Na nchi itaomboleza kwa sauti, kila ukoo peke yake; ukoo wa nyumba ya Daudi peke yake, na wanawake wao peke yao; ukoo wa nyumba ya Nathani+ peke yake, na wanawake wao peke yao; 13 ukoo wa nyumba ya Lawi+ peke yake, na wanawake wao peke yao; ukoo wa Washimei+ peke yake, na wanawake wao peke yao; 14 na koo zote zinazobaki, kila ukoo peke yake, na wanawake wao peke yao.

13 “Siku hiyo kisima kitafunguliwa kwa ajili ya nyumba ya Daudi na wakaaji wa Yerusalemu ili kuwasafisha dhambi na uchafu.+

2 “Siku hiyo,” asema Yehova wa majeshi, “nitafuta majina ya sanamu kutoka nchini,+ nayo hayatakumbukwa tena; nami nitawaondoa kabisa manabii+ na pia roho ya uchafu kutoka nchini. 3 Na mtu akitoa unabii tena, baba yake na mama yake waliomzaa watamwambia, ‘Hutaishi, kwa sababu umesema uwongo katika jina la Yehova.’ Na baba yake na mama yake waliomzaa watamchoma kisu kwa sababu ya unabii wake.+

4 “Siku hiyo kila nabii ataonea aibu maono yake anapotabiri; nao hawatavaa vazi rasmi la manyoya+ ili kudanganya. 5 Naye atasema, ‘Mimi si nabii. Mimi ni mkulima, kwa sababu mtu fulani alininunua nilipokuwa kijana.’ 6 Na mtu akimuuliza, ‘Majeraha haya uliyo nayo katikati ya mabega yako* yametoka wapi?’ atajibu, ‘Nilijeruhiwa katika nyumba ya rafiki zangu.’”*

 7 “Ee upanga, amka umshambulie mchungaji wangu,+

Mshambulie rafiki yangu,” asema Yehova wa majeshi.

“Mpige mchungaji,+ acha kondoo watawanyike;*+

Nami nitaugeuza mkono wangu dhidi ya watu wa hali ya chini.”

 8 “Na katika nchi yote,” asema Yehova,

“Theluthi mbili za watu zitaangamizwa na kutoweka;*

Na theluthi moja itaachwa humo.

 9 Na theluthi hiyo moja nitaipitisha motoni;

Nami nitawasafisha kama fedha inavyosafishwa,

Na kuwajaribu kama dhahabu inavyojaribiwa.+

Wataliitia jina langu,

Nami nitawajibu.

Nitasema, ‘Wao ni watu wangu,’+

Nao watasema, ‘Yehova ni Mungu wetu.’”

14 “Tazama! Siku inakuja, siku ya Yehova, wakati ambapo nyara yenu* itagawanywa miongoni mwenu. 2 Nitayakusanya mataifa yote ili yapigane vita na Yerusalemu; na jiji hilo litatekwa na nyumba zitaporwa na wanawake watabakwa. Na nusu ya wakaaji wa jiji hilo watapelekwa uhamishoni, lakini watakaobaki jijini hawataangamizwa.

3 “Yehova atatoka na kupigana vita na mataifa hayo+ kama anavyopigana katika siku ya vita.+ 4 Siku hiyo miguu yake itasimama kwenye Mlima wa Mizeituni,+ unaotazamana na jiji la Yerusalemu upande wa mashariki; na Mlima wa Mizeituni utagawanyika katikati, kuanzia mashariki* mpaka magharibi,* na bonde kubwa sana litatokea; na nusu ya mlima huo itaelekea kaskazini, na nusu nyingine kusini. 5 Mtakimbilia kwenye bonde la milima yangu, kwa maana bonde la milima hiyo litafika mpaka Aseli. Mtalazimika kukimbia kama mlivyokimbia kwa sababu ya tetemeko la ardhi katika siku za utawala wa Mfalme Uzia wa Yuda.+ Na Yehova Mungu wangu atakuja, na watakatifu wote watakuwa pamoja naye.+

6 “Siku hiyo hakutakuwa na nuru yenye thamani+—vitu vitagandishwa.* 7 Nayo itakuwa siku inayojulikana kuwa siku ya Yehova.+ Haitakuwa mchana, wala haitakuwa usiku; na jioni kutakuwa na nuru. 8 Siku hiyo maji yaliyo hai+ yatatiririka kutoka Yerusalemu,+ nusu yataelekea kwenye bahari ya mashariki*+ na nusu yataelekea kwenye bahari ya magharibi.*+ Hilo litatukia wakati wa kiangazi na wa baridi kali. 9 Na Yehova atakuwa Mfalme juu ya dunia yote.+ Siku hiyo Yehova atakuwa Mungu pekee,+ na jina lake litakuwa ndilo jina pekee.+

10 “Nchi yote itakuwa kama Araba,+ kuanzia Geba+ mpaka Rimoni+ upande wa kusini wa Yerusalemu; na jiji la Yerusalemu litainuka na kukaliwa na watu,+ kuanzia Lango la Benjamini+ mpaka kwenye Lango la Kwanza, mpaka kwenye Lango la Pembeni, na kuanzia Mnara wa Hananeli+ mpaka kwenye mashinikizo ya divai* ya mfalme. 11 Na watu watakaa jijini humo; hakutakuwa tena na laana ya uharibifu,+ na watu watakaa Yerusalemu kwa usalama.+

12 “Na huu ndio ugonjwa hatari ambao Yehova atawaletea watu wote wanaopigana vita na Yerusalemu:+ Miili yao itaoza wakiwa wamesimama, macho yao yataoza yakiwa kwenye matundu yake, na ndimi zao zitaoza vinywani mwao.

13 “Siku hiyo msukosuko kutoka kwa Yehova utaenea sana miongoni mwao; na kila mtu ataukamata mkono wa mwenzake, na mkono wake utaushambulia mkono wa mwenzake.*+ 14 Watu wa Yuda pia watashiriki katika vita huko Yerusalemu; na utajiri wa mataifa yote jirani utakusanywa, dhahabu na fedha na mavazi kwa wingi sana.+

15 “Na ugonjwa hatari wa aina hiyo utawashambulia pia farasi, nyumbu, ngamia, punda, na mifugo yote iliyo katika kambi hizo.

16 “Kila mtu atakayebaki kutoka katika mataifa yote yatakayoshambulia Yerusalemu atapanda mwaka baada ya mwaka+ kwenda Yerusalemu kumwinamia* Mfalme, Yehova wa majeshi,+ na kusherehekea Sherehe ya Vibanda.*+ 17 Lakini ikiwa taifa lolote miongoni mwa mataifa yaliyo duniani halitapanda kwenda Yerusalemu kumwinamia Mfalme, Yehova wa majeshi, mvua haitanyesha katika taifa hilo.+ 18 Na ikiwa taifa la Misri halitapanda kwenda Yerusalemu na kuingia humo, halitapata mvua. Badala yake, litashambuliwa na ugonjwa hatari ambao Yehova anauleta kwa mataifa ambayo hayapandi kwenda kusherehekea Sherehe ya Vibanda. 19 Hiyo ndiyo itakayokuwa adhabu kwa sababu ya dhambi ya Misri na dhambi ya mataifa yote ambayo hayatapanda kwenda kusherehekea Sherehe ya Vibanda.

20 “Siku hiyo maneno ‘Utakatifu ni wa Yehova!’+ yataandikwa kwenye kengele za farasi. Na vyungu vya kupikia*+ vilivyo katika nyumba ya Yehova vitakuwa kama mabakuli+ yaliyo mbele ya madhabahu. 21 Na kila chungu cha kupikia* kilicho Yerusalemu na Yuda kitakuwa kitakatifu na kitakuwa cha Yehova wa majeshi, na wale wote wanaotoa dhabihu wataingia na kutumia baadhi ya vyungu hivyo kuchemshia. Siku hiyo hakutakuwa tena na Mkanaani* katika nyumba ya Yehova wa majeshi.”+

Maana yake “Yehova Amekumbuka.”

Au “rudini.”

Angalia Nyongeza B15.

Yaani, ambalo halijazingirwa na kuta.

Tnn., “kwenye pande nne za mbingu.”

Tnn., “baada ya utukufu.”

Au “analigusa jicho langu.”

Au “wanadamu.”

Au “hatia yako.”

Au “majoho ya kifahari.”

Au “kusimamia; kulinda.”

Au “uwanda.”

Tnn., “vitu vidogo.”

Tnn., “jiwe, mkebe.”

Yaani, matawi yaliyojaa zeituni.

Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.

Tnn., “Ni efa inayotoka.” Efa inatumiwa hapa kurejelea chombo au kikapu kilichotumiwa kupima kipimo cha efa. Efa ya nafaka ilikuwa karibu kilogramu 13. Angalia Nyongeza B14.

Yaani, Babilonia.

Au “taji lenye utukufu.”

Yaani, kati ya cheo chake akiwa mtawala na cheo chake akiwa kuhani.

Au “taji lenye utukufu.”

Au “ukumbusho.”

Angalia Nyongeza B15.

Tnn., “wautulize uso wa Yehova.”

Au “hekalu la.”

Tnn., “mtoto asiye na baba.”

Au labda, “jiwe gumu,” kama vile jiwe la msasa.

Au “mafundisho.”

Au “uaminifu.”

Tnn., “kwa sababu ya wingi wa siku.”

Au “nchi ya mawio ya jua na nchi ya machweo ya jua.”

Au “uaminifu.”

Au “Iweni jasiri.”

Au “Iweni jasiri.”

Tnn., “tukautulize uso wa Yehova.”

Tnn., “kuutuliza uso wa Yehova.”

Au “upindo wa vazi.”

Tnn., “mwanamume Myahudi.”

Tnn., “litapumzika.”

Au “ngome.”

Shehe alikuwa mkuu wa kabila.

Au “mkandamizaji.”

Inaonekana ni mateso ya watu wake.

Au “naye ni mshindi; na ameokolewa.”

Au “punda dume.”

Tnn., “nitamkanyaga.”

Yaani, kama mshale.

Au “miungu ya familia; sanamu.”

Au “zimesema mambo ya uchawi; mazingaombwe.”

Au “waaguzi.”

Tnn., “mabeberu.”

Tnn., “Mnara wa pembeni unatoka kwake,” unafananisha mtu muhimu au wa maana sana; kiongozi.

Tnn., “Kigingi kinatoka kwake,” kinafananisha mtegemezaji; mtawala.”

Au “msimamizi wa watumwa.”

Au “wanasimba wenye manyoya marefu shingoni.”

Tnn., “wakanipimia.”

Tnn., “litafifia.”

Au “pumzi.”

Au “bakuli linalosababisha.”

Au “lenye kulemea.”

Shehe alikuwa mkuu wa kabila.

Au “mahali pake panapostahili.”

Au “fahari ya.”

Au “fahari ya.”

Au “aliye dhaifu zaidi.”

Tnn., “katikati ya mikono yako.” Yaani, kifuani au mgongoni.

Au “wale wanaonipenda.”

Au “kundi la kondoo litawanyike.”

Au “zitakufa.”

Yaani, jiji linalotajwa katika mstari wa 2.

Au “mawio ya jua.”

Tnn., “kwenye ile bahari.”

Au “vitakakamazwa,” kana kwamba vimekakamazwa na baridi.

Yaani, Bahari ya Chumvi.

Yaani, Bahari ya Mediterania.

Au “mitungi ya kushinikizia divai.”

Au “mtu atamshambulia mwenzake.”

Au “kumwabudu.”

Au “Vibanda vya Muda.”

Au “vyungu vya kupikia vyenye mdomo mpana.”

Au “chungu cha kupikia chenye mdomo mpana.”

Au labda, “mfanyabiashara.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki