Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt Waebrania 1:1-13:25
  • Waebrania

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Waebrania
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Waebrania

KWA WAEBRANIA

1 Zamani za kale, Mungu alizungumza na mababu zetu kupitia manabii katika pindi nyingi na kwa njia nyingi.+ 2 Lakini sasa mwishoni mwa siku hizi amezungumza nasi kupitia Mwana,+ aliyemweka rasmi kuwa mrithi wa vitu vyote,+ na kupitia kwake aliifanya mifumo ya mambo.*+ 3 Yeye ndiye mng’ao wa utukufu wa Mungu+ na mfano kamili wa utu wake,+ naye hutegemeza vitu vyote kwa neno la nguvu zake. Na baada ya kuzitakasa dhambi zetu,+ aliketi kwenye mkono wa kuume wa Ukuu huko juu.+ 4 Kwa hiyo amekuwa bora kuliko malaika,+ kwa maana amerithi jina bora kabisa kuliko lao.+

5 Kwa mfano, Mungu aliwahi kumwambia nani kati ya malaika: “Wewe ni mwanangu; leo nimekuwa baba yako”?+ Na tena: “Nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu”?+ 6 Lakini anapomleta tena Mzaliwa wake wa kwanza+ katika dunia inayokaliwa, anasema: “Malaika wote wa Mungu na wamsujudie.”*

7 Pia, anasema kuhusu malaika: “Huwafanya malaika wake kuwa roho, na wahudumu wake*+ kuwa mwali wa moto.”+ 8 Lakini kumhusu Mwana, anasema: “Mungu ni kiti chako cha ufalme+ milele na milele, na fimbo ya Ufalme wako ni fimbo ya unyoofu.* 9 Ulipenda uadilifu, nawe ukachukia uasi sheria. Ndiyo sababu Mungu, Mungu wako, amekutia mafuta+ kwa mafuta ya kushangilia kuliko wenzako.”+ 10 Na: “Hapo mwanzoni, Ee Bwana, uliiweka misingi ya dunia, na mbingu ni kazi za mikono yako. 11 Hizo zitaangamia, lakini wewe utadumu; na zote zitachakaa kama vazi, 12 nawe utazikunja kama kanzu, kama vazi, nazo zitabadilishwa. Lakini wewe ni yuleyule, na miaka yako haitafikia mwisho kamwe.”+

13 Lakini amewahi kumwambia malaika yupi hivi: “Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwaweke maadui wako kuwa kiti cha miguu yako”?+ 14 Je, wao wote si roho kwa ajili ya utumishi mtakatifu,*+ waliotumwa kuhudumu kwa ajili ya wale watakaorithi wokovu?

2 Hiyo ndiyo sababu ni lazima tuyakazie uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo tuliyosikia,+ ili tusipeperushwe kamwe.+ 2 Kwa maana ikiwa neno lililosemwa kupitia malaika+ lilikuwa hakika, na kila kosa na tendo la kutotii liliadhibiwa kupatana na haki,+ 3 je, sisi tutaponyoka ikiwa tumepuuza wokovu huo mkuu?+ Kwa kuwa ulianza kusemwa kupitia Bwana wetu+ nasi tukathibitishiwa na wale waliomsikia, 4 huku Mungu akijiunga katika kutoa ushahidi kwa ishara na mambo ya ajabu* na matendo mbalimbali yenye nguvu+ na roho takatifu iliyotolewa kulingana na mapenzi yake.+

5 Kwa maana dunia inayokaliwa inayokuja,+ ambayo tunazungumza kuihusu hajaitiisha chini ya malaika. 6 Lakini mahali fulani shahidi mmoja alisema: “Mwanadamu ni nini hivi kwamba unamweka akilini, au mwana wa mtu hivi kwamba unamtunza?+ 7 Ulimfanya awe mdogo kidogo kuliko malaika; ulimvika taji kwa utukufu na heshima, na kumweka juu ya kazi za mikono yako. 8 Ulivitiisha vitu vyote chini ya miguu yake.”+ Kwa kuvitiisha vitu vyote chini yake,+ Mungu hakuacha kitu chochote kisichotiishwa chini yake.+ Ingawa hivyo, bado hatuoni vitu vyote vikiwa vimetiishwa chini yake.+ 9 Lakini tunamwona Yesu, aliyefanywa kuwa mdogo kidogo kuliko malaika,+ sasa amevikwa taji la utukufu na heshima kwa kupatwa na kifo,+ ili kwa fadhili zisizostahiliwa za Mungu aonje kifo kwa ajili ya kila mtu.+

10 Kwa maana ilifaa kwamba yule ambaye kwa ajili yake na kupitia kwake vitu vyote vipo, katika kuleta wana wengi kwenye utukufu,+ alipaswa kumfanya Wakili Mkuu wa wokovu wao+ awe mkamilifu kupitia mateso.+ 11 Kwa maana yule anayetakasa na wale wanaotakaswa+ pia wote hutokana na mmoja,+ na kwa sababu hiyo yeye haoni aibu kuwaita ndugu,+ 12 kama anavyosema: “Nitalitangaza jina lako kwa ndugu zangu; katikati ya kutaniko nitakusifu kwa wimbo.”+ 13 Na tena: “Nitamtegemea yeye.”+ Na tena: “Tazama! Mimi na watoto wadogo, ambao Yehova* alinipa.”+

14 Basi, kwa kuwa “watoto wadogo” ni washiriki wa damu na mwili, vivyo hivyo yeye pia aliyashiriki mambo hayo,+ ili kupitia kifo chake amwangamize yule aliye na uwezo wa kusababisha kifo,+ yaani, Ibilisi,+ 15 na ili awaweke huru* wale wote waliokuwa chini ya utumwa katika maisha yao yote kwa kuogopa kifo.+ 16 Kwa maana kwa kweli yeye hawasaidii malaika, bali anasaidia uzao wa* Abrahamu.+ 17 Kwa hiyo alipaswa kuwa kama “ndugu” zake katika mambo yote,+ ili awe kuhani mkuu mwenye rehema na mwaminifu katika mambo yanayohusiana na Mungu, ili atoe dhabihu ya upatanisho*+ kwa ajili ya dhambi za watu.+ 18 Kwa kuwa yeye mwenyewe aliteseka alipokuwa akijaribiwa,+ anaweza kuwasaidia wale wanaojaribiwa.+

3 Kwa hiyo, ndugu watakatifu, washiriki wa mwito* wa mbinguni,+ mfikirieni mtume na kuhani mkuu tunayemkubali*—Yesu.+ 2 Alikuwa mwaminifu kwa Yule aliyemchagua,+ kama vile Musa alivyokuwa pia katika nyumba yote ya Mungu.+ 3 Kwa maana huyo* anastahili utukufu zaidi+ kuliko Musa, kwa kuwa yule anayejenga nyumba ana heshima kuliko nyumba yenyewe. 4 Bila shaka, kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yule aliyevijenga vitu vyote ni Mungu. 5 Sasa Musa alikuwa mtumishi mwaminifu katika nyumba yote ya Huyo akiwa ushuhuda* wa mambo ambayo yangesemwa baadaye, 6 lakini Kristo alikuwa mwaminifu akiwa mwana+ juu ya nyumba ya Mungu. Sisi ni nyumba Yake,+ ikiwa kwa kweli tunashikilia imara uhuru wetu wa kusema na tumaini ambalo tunajisifia mpaka mwisho.

7 Kwa hiyo, kama vile roho takatifu inavyosema,+ “Leo ikiwa mtaisikiliza sauti yake, 8 msiifanye mioyo yenu kuwa migumu kama ule wakati wa kusababisha hasira kali, kama siku ile ya jaribu nyikani,+ 9 ambayo mababu zenu waliniweka kwenye jaribu, na kunipima, ingawa waliona matendo yangu kwa miaka 40.+ 10 Ndiyo sababu nilichukizwa na kizazi hiki, nikasema: ‘Wao hupotoka sikuzote katika mioyo yao, nao hawazijui njia zangu.’ 11 Kwa hiyo niliapa kwa hasira yangu: ‘Hawataingia katika pumziko langu.’”+

12 Jihadharini, akina ndugu, ili moyo mwovu unaokosa imani usisitawi ndani ya yeyote kati yenu kwa kujiondoa kwa Mungu aliye hai;+ 13 lakini endeleeni kutiana moyo kila siku, maadamu inaitwa “Leo,”+ ili yeyote kati yenu asifanywe kuwa mgumu kwa nguvu za udanganyifu za dhambi. 14 Kwa maana kwa kweli tunakuwa washiriki wa* Kristo ikiwa tu tunashikilia imara mpaka mwisho uhakika tuliokuwa nao mwanzoni.+ 15 Kama inavyosemwa, “Leo ikiwa mtaisikiliza sauti yake, msiifanye mioyo yenu kuwa migumu kama ule wakati wa kusababisha hasira kali.”+

16 Kwa maana ni nani waliosikia na bado wakamchochea kuwa na hasira kali? Kwa kweli, je, si wale wote waliotoka Misri chini ya Musa?+ 17 Zaidi ya hayo, Mungu alichukizwa na akina nani kwa miaka 40?+ Je, si wale waliotenda dhambi, ambao maiti zao zilianguka nyikani?+ 18 Naye aliapa kwa akina nani kwamba hawataingia katika pumziko lake? Je, si wale waliotenda kwa kutotii? 19 Kwa hiyo tunaona kwamba hawakuingia kwa sababu walikosa imani.+

4 Kwa hiyo, kwa kuwa ahadi ya kuingia katika pumziko lake bado ipo, acheni tuwe macho* ili yeyote kati yenu asionekane amepungukiwa.+ 2 Kwa maana sisi pia tumetangaziwa habari njema,+ kama walivyotangaziwa; lakini neno walilosikia halikuwaletea faida, kwa sababu hawakuunganishwa kwa imani pamoja na wale waliosikia. 3 Kwa maana sisi ambao tumeonyesha imani tunaingia katika pumziko, kama alivyosema: “Kwa hiyo niliapa kwa hasira yangu, ‘Hawataingia katika pumziko langu,’”+ ingawa kazi zake zilimalizika tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu.+ 4 Kwa maana mahali fulani amesema hivi kuhusu siku ya saba: “Na Mungu akapumzika siku ya saba kutoka katika kazi zake zote,”+ 5 na hapa tena anasema: “Hawataingia katika pumziko langu.”+

6 Basi, kwa kuwa bado imebaki watu fulani waingie katika pumziko hilo, na wale ambao walitangaziwa kwanza habari njema hawakuingia kwa sababu ya kutotii,+ 7 yeye tena anaweka siku fulani kwa kusema baadaye katika zaburi ya Daudi, “Leo”; kama ilivyosemwa hapo juu, “Leo ikiwa mtaisikiliza sauti yake, msiifanye mioyo yenu kuwa migumu.”+ 8 Kwa maana ikiwa Yoshua+ aliwaingiza katika mahali pa pumziko, Mungu hangesema baadaye kuhusu siku nyingine. 9 Kwa hiyo bado limebaki pumziko la sabato kwa ajili ya watu wa Mungu.+ 10 Kwa maana mtu ambaye ameingia katika pumziko la Mungu, amepumzika pia kutoka kwenye kazi zake mwenyewe, kama Mungu alivyopumzika kutoka kwenye kazi zake.+

11 Kwa hiyo acheni tufanye yote tunayoweza ili kuingia katika pumziko hilo, ili yeyote asije akaanguka katika kielelezo kilekile cha kutotii.+ 12 Kwa maana neno la Mungu liko hai nalo ni lenye nguvu+ na lina makali kuliko upanga wowote wenye makali pande mbili+ nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi* na roho,* na viungo kutoka katika urojorojo, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo. 13 Na hakuna kiumbe kilichofichwa machoni pake,+ bali vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pa yule ambaye tunapaswa kutoa hesabu kwake.+

14 Basi, kwa kuwa tuna kuhani mkuu sana ambaye ameingia katika mbingu, Yesu Mwana wa Mungu,+ acheni tuendelee kumtangaza hadharani.+ 15 Kwa maana hatuna kuhani mkuu ambaye hawezi kuusikitikia udhaifu wetu,+ bali tuna yule ambaye amejaribiwa katika mambo yote kama tulivyojaribiwa, lakini hakutenda dhambi.+ 16 Basi na tukikaribie kiti cha ufalme cha fadhili zisizostahiliwa tukiwa na uhuru wa kusema,+ ili tupokee rehema na kupata fadhili zisizostahiliwa tunapohitaji msaada.*

5 Kwa maana kila kuhani mkuu anayechaguliwa miongoni mwa wanadamu huwekwa rasmi kwa ajili yao juu ya mambo yanayohusiana na Mungu,+ ili atoe zawadi na dhabihu kwa ajili ya dhambi.+ 2 Yeye anaweza kuwatendea kwa huruma* wale wasiojua na wanaokosea,* kwa sababu yeye pia anapambana* na udhaifu wake mwenyewe, 3 na hivyo ni lazima atoe dhabihu kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe kama vile anavyotoa kwa ajili ya dhambi za watu.+

4 Mtu hapati heshima hii kwa kupenda kwake mwenyewe, bali huipokea tu Mungu anapomwita, kama Haruni alivyoitwa.+ 5 Vivyo hivyo, pia Kristo hakujitukuza mwenyewe+ kwa kuwa kuhani mkuu, bali alitukuzwa na Yule aliyemwambia hivi: “Wewe ni mwanangu; leo nimekuwa baba yako.”+ 6 Kama vile pia anavyosema mahali pengine, “Wewe ni kuhani milele kwa mfano wa Melkizedeki.”+

7 Alipokuwa duniani,* Kristo alitoa dua na pia maombi, kwa vilio vyenye nguvu na machozi,+ kwa Yule aliyekuwa na uwezo wa kumwokoa kutoka katika kifo, naye akasikilizwa vizuri kwa sababu ya kumwogopa Mungu. 8 Ingawa alikuwa mwana, alijifunza kutii kutokana na mateso yaliyompata.+ 9 Na baada ya kufanywa kuwa mkamilifu,+ akawa na daraka la wokovu wa milele kwa ajili ya wote wanaomtii,+ 10 kwa sababu Mungu amemteua kuwa kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki.+

11 Tuna mengi ya kusema kumhusu na ni vigumu kuyafafanua, kwa sababu mmekuwa wazito wa kusikia. 12 Kwa maana, ingawa kufikia sasa* mnapaswa kuwa walimu, mnahitaji tena mtu awafundishe tangu mwanzo mambo ya msingi+ ya maneno matakatifu ya Mungu, nanyi mnahitaji maziwa tena, bali si chakula kigumu. 13 Kwa kuwa kila mtu anayeendelea kunywa maziwa hafahamu neno la uadilifu, kwa maana yeye ni mtoto mdogo.+ 14 Lakini chakula kigumu ni cha watu wakomavu, ambao wamezoeza nguvu zao za utambuzi* kwa kuzitumia ili kutofautisha mambo yaliyo sawa na mambo yasiyo sawa.

6 Kwa hiyo, kwa kuwa sasa tumeliacha nyuma fundisho la msingi+ kumhusu Kristo, na tusonge mbele kuelekea ukomavu,+ tusiweke msingi tena, yaani, kutubu matendo yaliyokufa na imani katika Mungu, 2 fundisho kuhusu aina mbalimbali za ubatizo na kuweka mikono,+ kufufuliwa kwa wafu+ na hukumu ya milele. 3 Na tutafanya hivyo ikiwa kwa kweli Mungu ataruhusu.

4 Kwa maana kuhusu wale ambao wakati fulani walikuwa kwenye nuru,+ na ambao wameonja zawadi ya bure ya kimbingu na ambao wamekuwa washiriki wa roho takatifu 5 na ambao wameonja neno zuri la Mungu na nguvu za mfumo wa mambo* unaokuja, 6 lakini wameanguka,+ haiwezekani kuwarudisha tena kwenye toba, kwa sababu wanamtundika tena mtini Mwana wa Mungu kwa ajili yao wenyewe na kumwaibisha hadharani.+ 7 Kwa maana udongo hupokea baraka kutoka kwa Mungu unapokunywa mvua inayonyesha juu yake mara kwa mara, na kisha huzaa mimea inayowanufaisha wale wanaoulima. 8 Lakini ukizaa miiba na michongoma, hukataliwa na huwa karibu kulaaniwa, na mwishowe huchomwa.

9 Lakini wapendwa, ingawa tunazungumza hivyo, tuna hakika mna hali bora, yaani, hali inayohusiana na wokovu. 10 Kwa maana Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake,+ kwa kuhudumu na kuendelea kuwahudumia watakatifu. 11 Lakini tunatamani kila mmoja wenu awe na bidii ileile ili kuwa na uhakikisho kamili wa tumaini+ mpaka mwisho,+ 12 ili msiwe goigoi,+ bali muwe waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.

13 Kwa maana Mungu alipotoa ahadi yake kwa Abrahamu, kwa kuwa hangeweza kuapa kwa yeyote aliye mkubwa zaidi, aliapa kwa jina lake mwenyewe,+ 14 akisema: “Hakika nitakubariki nami hakika nitaufanya uzao wako uwe mwingi.”+ 15 Basi, baada ya Abrahamu kuonyesha subira, aliipata ahadi hiyo. 16 Kwa maana watu huapa kwa mtu aliye mkubwa zaidi yao, na kiapo chao ndicho mwisho wa kila bishano, kwa kuwa ndicho uhakikisho wao wa kisheria.+ 17 Vivyo hivyo, Mungu alipoamua kuwaonyesha waziwazi warithi wa ile ahadi+ jinsi kusudi* lake lisivyobadilika, alitoa uhakikisho* kwa kiapo, 18 ili kupitia mambo mawili yasiyobadilika ambayo kuhusiana nayo Mungu hawezi kamwe kusema uwongo,+ sisi ambao tumekimbia kwenda katika kimbilio tutiwe moyo kabisa ili tushike imara tumaini lililowekwa mbele yetu. 19 Tuna tumaini hilo+ kama nanga ya nafsi,* likiwa hakika na imara, nalo huingia ndani ya pazia,+ 20 ambamo mtangulizi ameingia kwa ajili yetu, Yesu,+ ambaye amekuwa kuhani mkuu milele kama Melkizedeki.+

7 Kwa maana huyu Melkizedeki, mfalme wa Salemu, kuhani wa Mungu Aliye Juu Zaidi, alikutana na Abrahamu akirudi baada ya kuwaangamiza wafalme kisha akambariki,+ 2 naye Abrahamu akampa* sehemu ya kumi ya vitu vyote. Kwanza, jina lake linatafsiriwa “Mfalme wa Uadilifu,” kisha pia mfalme wa Salemu, yaani, “Mfalme wa Amani.” 3 Hana baba wala mama, hana ukoo, na hana mwanzo wa siku wala mwisho wa uzima, bali akiwa amefanywa kama Mwana wa Mungu, anadumu akiwa kuhani daima.*+

4 Oneni jinsi mtu huyu alivyokuwa mkuu, ambaye Abrahamu yule kichwa cha familia,* alimpa sehemu ya kumi kutoka kwa zile nyara bora.+ 5 Ni kweli, kulingana na Sheria, wazao wa Lawi+ ambao hupokea cheo chao cha ukuhani, wana amri ya kukusanya sehemu za kumi kutoka kwa watu,+ yaani, kutoka kwa ndugu zao, ingawa hao ni wazao wa* Abrahamu. 6 Lakini mtu huyu ambaye ukoo wake haukutokana nao, alichukua sehemu za kumi kutoka kwa Abrahamu na kumbariki yule aliyekuwa na zile ahadi.+ 7 Basi hakuna shaka kwamba mdogo hubarikiwa na mkubwa. 8 Na kwa upande mmoja, watu wanaokufa ndio wanaopokea sehemu za kumi, lakini kwa upande mwingine, ni mtu ambaye ushahidi unatolewa kwamba anaishi.+ 9 Na inaweza kusemwa kwamba hata Lawi, ambaye hupokea sehemu za kumi, amelipa sehemu za kumi kupitia Abrahamu, 10 kwa maana bado alikuwa mzao wa wakati ujao wa* babu yake wakati Melkizedeki alipokutana naye.+

11 Basi, ikiwa ukamilifu ungeweza kupatikana kupitia ukuhani wa Walawi+ (kwa maana ulikuwa sehemu ya Sheria ambayo watu walipewa), kungekuwa na umuhimu gani wa kuhani mwingine kusimama anayesemwa kuwa kwa mfano wa Melkizedeki+ na si kwa mfano wa Haruni? 12 Kwa kuwa ukuhani unabadilishwa, inakuwa muhimu kubadilisha Sheria pia.+ 13 Kwa maana mtu ambaye mambo haya yanasemwa kumhusu alitoka katika kabila lingine, na hakuna mtu wa kabila hilo ambaye amewahi kuhudumu kwenye madhabahu.+ 14 Kwa kuwa ni wazi kwamba Bwana wetu ametokana na Yuda,+ naye Musa hakusema kwamba makuhani wangetoka katika kabila hilo.

15 Na hilo linakuwa wazi hata zaidi kuhani mwingine+ anaposimama ambaye ni kama Melkizedeki,+ 16 ambaye amekuwa hivyo, si kupitia matakwa ya kisheria yanayotegemea uzao wa kimwili, bali kupitia nguvu za uzima usioweza kuharibika.+ 17 Kwa maana imesemwa katika ushahidi kumhusu: “Wewe ni kuhani milele kwa mfano wa Melkizedeki.”+

18 Basi, ile amri ya zamani inawekwa kando kwa sababu ni dhaifu na haifai.+ 19 Kwa maana Sheria haikufanya kitu chochote kiwe kikamilifu,+ lakini kuletwa kwa tumaini bora+ kulifanya hivyo, na kupitia tumaini hilo tunamkaribia Mungu.+ 20 Pia, kwa kuwa jambo hilo halikufanywa bila kiapo rasmi 21 (kwa kweli, kuna watu ambao wamekuwa makuhani bila kiapo rasmi, lakini huyu amekuwa kuhani kupitia kiapo kilichotolewa kumhusu na Yule aliyesema hivi: “Yehova* ameapa naye hatabadili nia yake,* ‘Wewe ni kuhani milele’”),+ 22 kwa hiyo Yesu amekuwa uhakikisho* wa agano bora.+ 23 Zaidi ya hayo, wengi walikuwa makuhani mmoja baada ya mwingine+ kwa sababu kifo kiliwazuia wasiendelee kuwa makuhani, 24 lakini kwa sababu yeye anaendelea kuishi milele,+ hakuna anayerithi ukuhani wake. 25 Basi anaweza pia kuwaokoa kikamili wale wanaomkaribia Mungu kupitia yeye, kwa sababu sikuzote yuko hai ili kuwaombea.+

26 Kwa maana inafaa tuwe na kuhani mkuu kama huyo ambaye ni mshikamanifu, asiye na hatia, asiye na unajisi,+ aliyetenganishwa na watenda dhambi, na aliyeinuliwa juu ya mbingu.+ 27 Tofauti na makuhani hao wakuu, hahitaji kutoa dhabihu kila siku,+ kwanza kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe kisha kwa ajili ya dhambi za watu,+ kwa sababu alifanya hivyo mara moja kwa wakati wote alipojitoa mwenyewe.+ 28 Kwa maana Sheria huweka rasmi watu walio na udhaifu wawe makuhani wakuu,+ lakini neno la kiapo+ rasmi baada ya Sheria humweka rasmi Mwana, ambaye amefanywa kuwa mkamilifu+ milele.

8 Sasa jambo kuu tunalosema ni hili: Sisi tuna kuhani mkuu wa namna hii,+ naye ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Ukuu mbinguni,+ 2 mhudumu* wa mahali patakatifu+ na wa hema la kweli, ambalo limesimamishwa na Yehova,* na si mwanadamu. 3 Kwa maana kila kuhani mkuu huwekwa rasmi ili kutoa zawadi na dhabihu; basi ilikuwa lazima huyu pia awe na kitu cha kutoa.+ 4 Ikiwa angekuwa duniani, hangekuwa kuhani,+ kwa sababu tayari kuna watu wanaotoa zawadi kulingana na Sheria. 5 Watu hao hufanya utumishi mtakatifu kwa mfano wa uhalisi na kivuli+ cha vitu vya mbinguni;+ kama vile Musa, alipokuwa karibu kujenga hema, alipewa amri na Mungu: Kwa kuwa Mungu anasema: “Hakikisha kwamba unatengeneza vitu vyote kwa kufuata kielelezo ulichoonyeshwa mlimani.”+ 6 Lakini sasa Yesu amepata huduma iliyo bora* zaidi kwa sababu yeye pia ni mpatanishi+ wa agano lililo bora+ kwa kulinganishwa, ambalo limefanywa imara kisheria juu ya ahadi zilizo bora.+

7 Ikiwa agano la kwanza halingekuwa na kosa, hakungekuwa na haja ya agano la pili.+ 8 Kwa maana anaona hatia ya watu anaposema: “‘Tazama! Siku zinakuja,’ asema Yehova,* ‘nitakapofanya agano jipya pamoja na nyumba ya Israeli na nyumba ya Yuda. 9 Halitakuwa kama agano nililofanya pamoja na mababu zao siku niliyowashika mkono na kuwaongoza kutoka nchini Misri,+ kwa sababu hawakuendelea kulishika agano langu, basi nikaacha kuwajali,’ asema Yehova.*

10 “‘Kwa maana hili ndilo agano nitakalofanya pamoja na nyumba ya Israeli baada ya siku hizo,’ asema Yehova.* ‘Nitazitia sheria zangu katika akili yao, nami nitaziandika katika mioyo yao.+ Nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.+

11 “‘Nao hawatafundishana tena kila mtu na raia mwenzake na kila mtu na ndugu yake, wakisema: “Mjue Yehova!”* Kwa maana wote watanijua, kuanzia mdogo zaidi mpaka aliye mkubwa zaidi miongoni mwao. 12 Kwa maana nitaonyesha rehema kwa matendo yao yasiyo ya uadilifu, nami sitazikumbuka tena dhambi zao.’”+

13 Anaposema “agano jipya,” amelifanya lile la zamani lichakae.+ Basi kile kilichochakaa na kuzeeka kiko karibu kutoweka.+

9 Basi, kwa upande wake, lile agano la zamani lilikuwa na matakwa ya kisheria kwa ajili ya utumishi mtakatifu na mahali pake patakatifu+ duniani. 2 Kwa maana chumba cha kwanza cha hema kilijengwa, na ndani yake mlikuwa na kinara cha taa+ na meza na mikate ya toleo;*+ nacho kinaitwa Mahali Patakatifu.+ 3 Lakini nyuma ya pazia la pili+ kulikuwa na chumba cha hema kilichoitwa Patakatifu Zaidi.+ 4 Hicho kilikuwa na chetezo cha dhahabu+ na sanduku la agano+ likiwa limefunikwa kabisa kwa dhahabu,+ ambalo ndani yake mlikuwa na mtungi wa dhahabu wenye mana,+ fimbo ya Haruni iliyochipuka,+ na yale mabamba+ ya agano; 5 na juu yake palikuwa na wale makerubi wenye utukufu waliokifunika kile kifuniko cha upatanisho.*+ Lakini sasa si wakati wa kuzungumzia mambo hayo kirefu.

6 Baada ya vitu hivyo kujengwa kwa njia hiyo, makuhani huingia katika chumba cha kwanza cha hema kwa ukawaida ili kutoa utumishi mtakatifu;+ 7 lakini kuhani mkuu huingia ndani ya chumba cha pili akiwa peke yake mara moja kwa mwaka,+ akiwa na damu,+ ambayo huitoa kwa ajili yake mwenyewe+ na kwa ajili ya dhambi ambazo watu+ walifanya bila kujua. 8 Hivyo roho takatifu hufanya iwe wazi kwamba njia ya kuingia mahali patakatifu bado haikuwa imefunuliwa lile hema la zamani lilipokuwa limesimama.+ 9 Hema hili ni mfano kwa ajili ya wakati huu,+ na kulingana na mpango huu, zawadi na dhabihu zinatolewa.+ Hata hivyo, haziwezi kufanya dhamiri ya mtu anayefanya utumishi mtakatifu iwe kamilifu.+ 10 Zinahusu vyakula na vinywaji tu na njia mbalimbali za kujisafisha kisherehe.*+ Hayo yalikuwa matakwa ya kisheria kuhusu mwili+ nayo yalifuatwa mpaka wakati uliowekwa wa kunyoosha mambo.

11 Hata hivyo, Kristo alipokuja akiwa kuhani mkuu wa mambo mema ambayo tayari yamefanyika, aliingia katika hema kubwa na kamilifu zaidi ambalo halikutengenezwa kwa mikono, yaani, si la uumbaji huu. 12 Aliingia mahali patakatifu, si kwa damu ya mbuzi na ya ng’ombe dume wachanga, bali kwa damu yake mwenyewe,+ mara moja kwa wakati wote, na kupata ukombozi wa* milele kwa ajili yetu.+ 13 Kwa maana ikiwa damu ya mbuzi na ya ng’ombe dume+ na majivu ya ndama jike yaliyonyunyizwa juu ya wale ambao wametiwa unajisi hutakasa ili kuusafisha mwili,+ 14 je, damu ya Kristo,+ ambaye kupitia roho inayodumu milele alijitoa mwenyewe kwa Mungu bila dosari, haitazisafisha hata zaidi dhamiri zetu kutoka katika matendo yaliyokufa+ ili tumtolee utumishi mtakatifu Mungu aliye hai?+

15 Hiyo ndiyo sababu yeye ni mpatanishi wa agano jipya,+ ili kwa sababu kifo kimetokea kusudi waachiliwe huru kupitia fidia+ kutoka kwenye makosa chini ya agano la zamani, wale ambao wameitwa waipokee ahadi ya urithi unaodumu milele.+ 16 Kwa maana palipo na agano, kifo cha mwanadamu anayefanya agano kinahitaji kuthibitishwa, 17 kwa sababu agano huwa halali kifo kinapotokea, kwa kuwa halitumiki ikiwa mwanadamu anayefanya agano bado yuko hai. 18 Kwa hiyo, lile agano la zamani halikuanza kutumika* bila damu. 19 Kwa maana Musa alipowatajia watu wote kila amri ya Sheria, alichukua damu ya wale ng’ombe dume wachanga na ya wale mbuzi, pamoja na maji, sufu nyekundu, na hisopo, na kukinyunyizia kile kitabu* na watu wote, 20 akisema: “Hii ndiyo damu ya agano ambalo Mungu amewaamuru mlishike.”+ 21 Vilevile alilinyunyizia damu lile hema na vyombo vyote vya utumishi mtakatifu.*+ 22 Ndiyo, kulingana na Sheria karibu vitu vyote husafishwa kwa damu,+ na hakuna msamaha unaopatikana bila kumwaga damu.+

23 Kwa hiyo, ilikuwa muhimu kwa mifano ya uhalisi+ wa vitu vilivyo mbinguni kusafishwa kwa njia hiyo,+ lakini vitu vya mbinguni vinahitaji dhabihu zilizo bora zaidi. 24 Kwa maana Kristo hakuingia mahali patakatifu palipotengenezwa kwa mikono,+ ambapo ni mfano wa uhalisi,+ bali aliingia mbinguni kwenyewe,+ hivi kwamba sasa anaonekana mbele za* Mungu kwa ajili yetu.+ 25 Hilo halikufanywa ili ajitoe mwenyewe mara nyingi, kama kuhani mkuu anavyoingia mahali patakatifu mwaka baada ya mwaka+ akiwa na damu ambayo si yake mwenyewe. 26 La sivyo, ingekuwa lazima ateseke mara nyingi tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu. Lakini sasa amejifunua mara moja kwa wakati wote kwenye umalizio wa mifumo ya mambo* ili kuondoa dhambi kupitia dhabihu yake mwenyewe.+ 27 Na kama vile watu wamewekwa akiba kufa mara moja kwa wakati wote, lakini baada ya hapo wapokee hukumu, 28 vivyo hivyo pia Kristo alitolewa mara moja kwa wakati wote ili kubeba dhambi za wengi;+ na mara ya pili atakapotokea itakuwa bila dhambi,* naye ataonwa na wale wanaomtazamia kwa bidii kwa ajili ya wokovu wao.+

10 Kwa kuwa Sheria ina kivuli+ cha mambo mema yatakayokuja,+ lakini si uhalisi wa mambo hayo, haiwezi* kamwe kwa dhabihu zilezile zinazotolewa mwaka baada ya mwaka, kuwafanya wale wanaokaribia wawe wakamilifu.+ 2 La sivyo, je, dhabihu hazingekoma kutolewa, kwa sababu wale wanaotoa utumishi mtakatifu baada ya kusafishwa mara moja hawangehisi wana dhambi tena? 3 Kinyume chake, dhabihu hizo ni kikumbusho cha dhambi mwaka baada ya mwaka,+ 4 kwa maana damu ya ng’ombe dume na ya mbuzi haiwezi kuondoa dhambi.

5 Basi anapokuja katika ulimwengu anasema: “‘Hukutaka dhabihu na toleo, bali ulinitayarishia mwili. 6 Hukukubali dhabihu nzima za kuteketezwa na dhabihu za dhambi.’+ 7 Kisha nikasema: ‘Tazama! nimekuja (katika kitabu cha kukunjwa imeandikwa kunihusu) kufanya mapenzi yako, Ee Mungu.’”+ 8 Kwanza aliposema: “Hukutaka wala hukukubali dhabihu, matoleo, dhabihu nzima za kuteketezwa, na dhabihu za dhambi”—dhabihu zinazotolewa kulingana na Sheria— 9 kisha anasema: “Tazama! nimekuja kufanya mapenzi yako.”+ Anaondoa la kwanza ili asimamishe la pili. 10 Kwa “mapenzi” hayo+ sisi tumetakaswa kupitia toleo la mwili wa Yesu Kristo mara moja kwa wakati wote.+

11 Pia, kila kuhani husimama mahali pake siku kwa siku ili kutoa utumishi mtakatifu*+ na kutoa mara nyingi dhabihu zilezile,+ ambazo haziwezi kuondoa kabisa dhambi.+ 12 Lakini mtu huyu alitoa dhabihu moja kwa ajili ya dhambi daima na kuketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu,+ 13 tangu wakati huo akisubiri mpaka adui zake wawekwe kuwa kiti cha miguu yake.+ 14 Kwa maana kupitia toleo moja la dhabihu amewafanya wale wanaotakaswa wawe wakamilifu+ daima. 15 Zaidi ya hayo, roho takatifu pia inatutolea ushahidi, kwa maana baada ya kusema: 16 “‘Hili ndilo agano nitakalofanya pamoja nao baada ya siku hizo,’ asema Yehova.* ‘Nitazitia sheria zangu katika mioyo yao, nami nitaziandika katika akili zao.’”+ 17 Kisha inasema: “Nami sitazikumbuka tena dhambi zao na matendo yao ya kuasi sheria.”+ 18 Sasa kunapokuwa na msamaha wa mambo hayo, hakuna tena toleo kwa ajili ya dhambi.

19 Kwa hiyo, akina ndugu, kwa kuwa tuna ujasiri* wa njia ya kuingia katika mahali patakatifu+ kwa damu ya Yesu, 20 aliyotufungulia* kuwa njia mpya na yenye uzima kupitia lile pazia,+ yaani, mwili wake, 21 na kwa kuwa tuna kuhani mkuu aliye juu ya nyumba ya Mungu,+ 22 acheni tukaribie tukiwa na mioyo minyoofu na imani kamili, mioyo yetu ikiwa imenyunyizwa na kuwa safi kutokana na dhamiri yenye uovu+ na miili yetu ikiwa imeoshwa kwa maji safi.+ 23 Acheni tushike imara tangazo la hadharani la tumaini letu bila kuyumbayumba,+ kwa maana yule aliyeahidi ni mwaminifu. 24 Na acheni tufikiriane* ili kuchocheana* katika upendo na matendo mazuri,+ 25 bila kuacha kukutana pamoja,+ kama wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo,+ na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile ikikaribia.+

26 Kwa maana tukiendelea kutenda dhambi kimakusudi baada ya kupokea ujuzi sahihi wa kweli,+ hakuna tena dhabihu yoyote iliyobaki kwa ajili ya dhambi,+ 27 bali kuna tarajio hakika linaloogopesha la hukumu na hasira inayowaka itakayowaangamiza wale wanaopinga.+ 28 Mtu yeyote ambaye ameipuuza Sheria ya Musa hufa bila huruma, kwa ushuhuda wa watu wawili au watatu.+ 29 Mnafikiri mtu ambaye amemkanyagia chini Mwana wa Mungu na ambaye ameiona kuwa yenye thamani ya kawaida tu damu ya agano+ ambayo kupitia hiyo alitakaswa, na ambaye ameidharau roho ya fadhili zisizostahiliwa, atapata adhabu kubwa kadiri gani?+ 30 Kwa maana tunamjua Yule aliyesema: “Kisasi ni changu; mimi nitalipa.” Na tena: “Yehova* atawahukumu watu wake.”+ 31 Ni jambo lenye kuogopesha kuanguka mikononi mwa Mungu aliye hai.

32 Hata hivyo, endeleeni kuzikumbuka siku za zamani ambazo, baada ya kupata nuru,+ mlivumilia pambano kubwa pamoja na mateso. 33 Nyakati fulani mlifunuliwa hadharani* kwa shutuma na dhiki pia, na nyakati fulani mlishiriki* pamoja na wale waliokuwa wakipatwa na mambo kama hayo. 34 Kwa maana mliwasikitikia wale waliokuwa gerezani na pia kwa shangwe mkakubali kuporwa mali zenu,+ mkijua kwamba ninyi wenyewe mna urithi* bora na wenye kudumu.+

35 Kwa hiyo, msiutupe ujasiri wenu,* ambao utathawabishwa sana.+ 36 Kwa kuwa mnahitaji uvumilivu,+ ili baada ya kufanya mapenzi ya Mungu, mpokee utimizo wa ile ahadi. 37 Kwa maana bado “muda kidogo sana,”+ na “yule anayekuja atafika naye hatakawia.”+ 38 “Lakini mwadilifu wangu ataishi kupitia imani,”+ naye “akirudi nyuma kwa kutetemeka, mimi sipendezwi* naye.”+ 39 Sasa sisi si namna ya watu wanaorudi nyuma kwenye maangamizi,+ bali sisi ni watu walio na imani ya kuhifadhi uhai wetu.*

11 Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa,+ uthibitisho ulio wazi* wa mambo halisi ambayo hayaonekani. 2 Kwa maana kupitia imani, watu wa nyakati za kale* walitolewa ushahidi.

3 Kwa imani tunatambua kwamba mifumo ya mambo* ilipangwa kwa utaratibu kwa neno la Mungu, hivi kwamba kile kinachoonekana, kimekuwapo kutokana na vitu visivyoonekana.

4 Kwa imani, Abeli alimtolea Mungu dhabihu ya thamani kubwa zaidi kuliko ile ya Kaini,+ na kupitia imani hiyo alitolewa ushahidi kwamba alikuwa mwadilifu, kwa kuwa Mungu alikubali* zawadi zake,+ na ingawa alikufa, bado anazungumza+ kupitia imani yake.

5 Kwa imani, Enoko+ alihamishwa ili asione kifo, naye hakupatikana popote kwa sababu Mungu alikuwa amemhamisha;+ kwa maana kabla ya kuhamishwa alikuwa ametolewa ushahidi kwamba amempendeza Mungu vema. 6 Isitoshe, bila imani haiwezekani kumpendeza Mungu vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kuwa yuko* na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.+

7 Kwa imani, Noa+ baada ya kuonywa na Mungu kuhusu mambo ambayo bado hayakuwa yameonekana,+ alimtii Mungu* kwa kujenga safina+ kwa ajili ya kuiokoa nyumba yake; na kupitia imani hiyo aliuhukumu ulimwengu,+ naye akawa mrithi wa uadilifu unaotokana na imani.

8 Kwa imani, Abrahamu+ alipoitwa alitii kwa kutoka na kwenda mahali ambapo angepokea kuwa urithi; aliondoka, ingawa hakujua mahali alipokuwa akienda.+ 9 Kwa imani aliishi akiwa mgeni katika nchi ya ahadi kama katika nchi ya kigeni,+ akiishi kwenye mahema+ pamoja na Isaka na Yakobo, warithi pamoja naye wa ahadi ileile.+ 10 Kwa maana alikuwa akingojea jiji lililo na misingi ya kweli, ambalo mbuni* na mjenzi wake ni Mungu.+

11 Kwa imani, Sara pia alipokea nguvu za kupata uzao,* ingawa alikuwa amepita umri,+ kwa kuwa alimwona kuwa mwaminifu* Yule aliyekuwa ameahidi. 12 Kwa sababu hiyo, kutoka kwa mwanamume mmoja, ambaye alikuwa kama mfu,+ walizaliwa watoto+ wengi kama nyota za mbinguni na wasiohesabika kama mchanga ulio kando ya bahari.+

13 Katika imani hawa wote walikufa, ingawa hawakupokea utimizo wa zile ahadi;+ bali waliziona kwa mbali+ na kuzikaribisha na kutangaza hadharani kwamba walikuwa wageni na wakaaji wa muda katika nchi.⁠ 14 Kwa maana wale wanaozungumza hivyo wanathibitisha kwamba wanatafuta kwa bidii mahali pao wenyewe. 15 Na bado, kama wangeendelea kukumbuka mahali walipokuwa wametoka,+ wangepata nafasi ya kurudi. 16 Lakini sasa wanajitahidi kufikia mahali bora zaidi, yaani, panapohusiana na mbinguni. Kwa hiyo, Mungu haoni aibu kuwahusu, anapoitwa Mungu wao,+ kwa maana ametayarisha jiji kwa ajili yao.+

17 Kwa imani, Abrahamu alipojaribiwa,+ ni kana kwamba alimtoa Isaka—mtu huyo aliyekuwa amezipokea ahadi kwa furaha alijaribu kumtoa mwana wake mzaliwa-pekee+— 18 ingawa alikuwa ameambiwa: “Ule utakaoitwa uzao* wako utapitia kwa Isaka.”+ 19 Lakini alifikia uamuzi kwamba Mungu angeweza kumfufua hata kutoka kwa wafu, naye alimpokea kutoka huko kwa njia ya mfano.+

20 Kwa imani pia, Isaka alimbariki Yakobo+ na Esau+ kuhusu mambo yatakayokuja.

21 Kwa imani, Yakobo alipokuwa karibu kufa,+ aliwabariki wana wawili wa Yosefu+ na akaabudu huku akiegemea juu ya fimbo yake.+

22 Kwa imani, Yosefu akikaribia mwisho wake, alizungumza kuhusu kutoka* kwa wana wa Israeli, naye akawapa maagizo* kuhusu mifupa* yake.+

23 Kwa imani, Musa alifichwa kwa miezi mitatu na wazazi wake baada ya kuzaliwa,+ kwa sababu waliona kwamba huyo mtoto mchanga alikuwa mwenye kupendeza+ nao hawakuliogopa agizo la mfalme.+ 24 Kwa imani, Musa alipokuwa mtu mzima,+ alikataa kuitwa mwana wa binti ya Farao,+ 25 akachagua kuteswa pamoja na watu wa Mungu badala ya kufurahia dhambi kwa muda, 26 kwa sababu aliona shutuma ya Kristo kuwa utajiri mkubwa kuliko hazina za Misri, kwa maana alikaza macho kwenye malipo ya thawabu. 27 Kwa imani aliondoka Misri,+ lakini hakuogopa hasira ya mfalme,+ kwa maana aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yule asiyeonekana.+ 28 Kwa imani alifanya sherehe ya Pasaka na kupaka damu, ili mwangamizaji asiwadhuru* wazaliwa wao wa kwanza.+

29 Kwa imani walipita katika Bahari Nyekundu kama kwenye nchi kavu,+ lakini Wamisri walipojaribu kupita wakamezwa.+

30 Kwa imani kuta za Yeriko zilianguka baada ya watu kuzizunguka kwa siku saba.+ 31 Kwa imani, Rahabu yule kahaba hakuangamia pamoja na wale waliokosa kutii, kwa sababu aliwapokea wale wapelelezi kwa amani.+

32 Nami nitasema nini zaidi? Kwa maana nitakosa wakati nikiendelea kusimulia kuhusu Gideoni,+ Baraka,+ Samsoni,+ Yeftha,+ Daudi,+ na vilevile Samweli+ na wale manabii wengine. 33 Kupitia imani walishinda falme,+ wakaleta uadilifu, wakapata ahadi,+ wakaziba vinywa vya simba,+ 34 wakazima nguvu za moto,+ wakaponyoka makali ya upanga,+ wakafanywa kuwa wenye nguvu kutoka kwenye hali ya udhaifu,+ wakawa mashujaa katika vita,+ wakayashinda kabisa majeshi ya wavamizi.+ 35 Wanawake waliwapokea wafu wao kupitia ufufuo,+ lakini watu wengine waliteswa kwa sababu hawakukubali kuachiliwa kupitia fidia fulani, ili waupate ufufuo ulio bora. 36 Ndiyo, wengine walipata jaribu lao kwa kudhihakiwa na kupigwa kwa mijeledi, naam, isitoshe, kwa kufungwa minyororo+ na magerezani.+ 37 Walipigwa mawe,+ walijaribiwa, walikatwa vipande viwili* kwa msumeno, walichinjwa kwa upanga,+ walitembea huku na huku wakiwa wamevaa ngozi za kondoo na ngozi za mbuzi,+ wakiwa katika uhitaji, katika dhiki,+ wakiteswa;+ 38 na ulimwengu haukuwafaa. Walitembea huku na huku katika majangwa na milima na mapango+ na mashimo ya dunia.

39 Na bado hawa wote, ingawa walitolewa ushahidi unaofaa kwa sababu ya imani yao, hawakupata utimizo wa ile ahadi, 40 kwa sababu Mungu aliona mapema kitu bora kwa ajili yetu,+ ili wasifanywe kuwa wakamilifu bila sisi.

12 Hivyo basi, kwa kuwa tuna wingu kubwa hivyo la mashahidi linalotuzunguka, acheni sisi pia tuondoe kila uzito na dhambi inayotutatanisha kwa urahisi,+ na tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu,+ 2 huku tukimtazama kwa makini Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu.+ Kwa sababu ya shangwe iliyowekwa mbele yake, alivumilia mti wa mateso,* akaidharau aibu, naye ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.+ 3 Kwa kweli, mfikirieni sana yule ambaye amevumilia maneno makali kama hayo kutoka kwa watenda dhambi+ kinyume cha faida zao wenyewe, ili msichoke na kukata tamaa.*+

4 Katika pambano lenu na dhambi, hamjapambana kamwe kufikia hatua ya kumwaga damu. 5 Nanyi mmesahau kabisa lile himizo linalosema nanyi kama wana: “Mwanangu, usiipuuze nidhamu kutoka kwa Yehova,* wala usikate tamaa anapokurekebisha; 6 kwa maana Yehova* huwatia nidhamu wale anaowapenda, kwa kweli, humpiga fimbo* kila mtu ambaye amempokea kuwa mwana.”+

7 Mnahitaji kuvumilia kama sehemu ya nidhamu* yenu. Mungu anawatendea ninyi kama wana.+ Kwa maana ni mwana gani ambaye hatiwi nidhamu na baba yake?+ 8 Lakini ikiwa ninyi nyote hamjashiriki katika kupokea nidhamu hii, kwa kweli ninyi ni watoto haramu, bali si wana. 9 Zaidi ya hayo, baba zetu wa kibinadamu* walikuwa wakitutia nidhamu, nasi tuliwapa heshima. Je, hatupaswi kujitiisha hata zaidi kwa Baba wa maisha yetu ya kiroho na kuishi?+ 10 Kwa maana walitutia nidhamu kwa muda mfupi kulingana na jinsi walivyoona kuwa inafaa, lakini yeye hufanya hivyo kwa faida yetu ili tuushiriki utakatifu wake.+ 11 Ni kweli, hakuna nidhamu inayoonekana kwa sasa kuwa yenye shangwe, bali inaumiza;* lakini baadaye hutokeza amani na uadilifu* kwa wale ambao wamezoezwa nayo.

12 Kwa hiyo, imarisheni mikono inayolegea na magoti yaliyo dhaifu,+ 13 nanyi endeleeni kuifanyia miguu yenu mapito yaliyonyooka,+ ili kile ambacho ni kilemavu kisiteguke, badala yake, kiponywe. 14 Fuatilieni amani pamoja na watu wote+ na utakaso*+ ambao bila huo hakuna mtu atakayemwona Bwana. 15 Iweni waangalifu kwamba yeyote asikose kupata fadhili zisizostahiliwa za Mungu, ili mzizi wowote wenye sumu usichipuke na kusababisha taabu na wengi watiwe unajisi nao;+ 16 na muwe waangalifu ili miongoni mwenu kusiwe na mwasherati* wala yeyote asiyethamini mambo matakatifu, kama Esau, aliyetoa haki zake za kuwa mzaliwa wa kwanza kwa kubadilishana na mlo mmoja.+ 17 Kwa kuwa mnajua kwamba baadaye alipotaka kuirithi baraka, alikataliwa; kwa maana, ingawa alijaribu kwa bidii kubadili fikira* kwa machozi,+ hakufaulu.*

18 Kwa maana hamkukaribia kitu kinachoweza kuguswa+ na ambacho kimewashwa moto,+ na wingu jeusi na giza zito na dhoruba,+ 19 na mlio wa tarumbeta+ na sauti ya maneno yanayosemwa,+ ambayo watu walipoisikia waliomba kwamba wasiambiwe neno lingine lolote.+ 20 Kwa maana hawakuweza kuivumilia amri hii: “Hata mnyama akiugusa mlima, lazima apigwe mawe.”+ 21 Pia, wonyesho huo ulikuwa wa kutisha sana hivi kwamba Musa akasema: “Ninaogopa na kutetemeka.”+ 22 Lakini ninyi mmeukaribia Mlima Sayuni,+ jiji la Mungu aliye hai, yaani, Yerusalemu la mbinguni,+ na makumi ya maelfu ya malaika 23 katika kusanyiko kuu,+ na kutaniko la wazaliwa wa kwanza ambao wameandikishwa mbinguni, na Mungu Mwamuzi wa wote,+ na maisha ya kiroho+ ya waadilifu ambao wamefanywa wakamilifu,+ 24 na Yesu mpatanishi+ wa agano jipya,+ na damu iliyonyunyizwa, ambayo husema kwa njia bora kuliko damu ya Abeli.+

25 Angalieni kwamba msikatae kumsikiliza* yule anayezungumza. Kwa maana ikiwa wale waliokataa kumsikiliza yule aliyetoa onyo kutoka kwa Mungu duniani hawakuponyoka, je, kweli sisi tutaponyoka ikiwa tutamwacha yule anayezungumza kutoka mbinguni?+ 26 Wakati huo sauti yake iliitikisa dunia,+ lakini sasa ameahidi: “Nitatikisa kwa mara nyingine tena, si dunia tu bali pia mbingu.”+ 27 Sasa maneno “kwa mara nyingine tena” yanaonyesha kuondolewa kwa vitu vinavyotikiswa, vitu vilivyotengenezwa, ili vitu ambavyo havitikiswi vibaki. 28 Kwa hiyo, kwa kuwa tutapokea Ufalme usioweza kutikiswa, acheni tuendelee kupokea fadhili zisizostahiliwa, ambazo zitatuwezesha kumtolea Mungu utumishi mtakatifu kwa njia inayokubalika, kwa kumwogopa Mungu na kumheshimu. 29 Kwa maana Mungu wetu ni moto unaoteketeza.+

13 Upendo wenu wa kindugu na uendelee.+ 2 Msisahau kuwakaribisha wageni,*+ kwa maana kwa kufanya hivyo watu fulani bila kujua waliwakaribisha malaika.+ 3 Wakumbukeni wale walio gerezani,*+ kana kwamba mmefungwa pamoja nao,+ na wale wanaoteswa, kwa kuwa ninyi pia mko katika mwili.* 4 Ndoa na iheshimiwe kati ya wote, na kitanda cha ndoa kisiwe na unajisi,+ kwa maana Mungu atawahukumu waasherati* na wazinzi.+ 5 Njia yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa,+ huku mkiridhika na vitu mlivyo navyo.*+ Kwa maana amesema: “Sitakuacha wala kukutupa kamwe.”+ 6 Ili tuwe hodari na kusema: “Yehova* ni msaidizi wangu; sitaogopa. Mwanadamu atanifanya nini?”+

7 Wakumbukeni wale wanaoongoza kati yenu,+ ambao wamelisema neno la Mungu kwenu, nanyi mnapotafakari matokeo ya mwenendo wao, igeni imani yao.+

8 Yesu Kristo ni yuleyule jana, leo, na milele.

9 Msipotoshwe na mafundisho mbalimbali yaliyo mageni, kwa maana ni bora moyo uimarishwe kwa fadhili zisizostahiliwa, bali si kwa vyakula,* ambavyo haviwanufaishi wale wanaojishughulisha navyo.+

10 Sisi tuna madhabahu ambayo wale wanaofanya utumishi mtakatifu katika hema hawana mamlaka ya kula kilicho juu yake.+ 11 Kwa maana miili ya wanyama ambao kuhani mkuu hupeleka damu yao ndani ya mahali patakatifu kama toleo la dhambi huteketezwa nje ya kambi.+ 12 Kwa hiyo, Yesu pia aliteseka nje ya lango la jiji+ ili awatakase watu kwa damu yake mwenyewe.+ 13 Basi, acheni twende kwake nje ya kambi, tukiibeba shutuma aliyoibeba,+ 14 kwa maana hapa hatuna jiji linalodumu, bali tunatafuta kwa bidii lile litakalokuja.+ 15 Kupitia yeye sikuzote na tumtolee Mungu dhabihu ya sifa,+ yaani, tunda la midomo yetu+ ambalo hulitangaza jina lake hadharani.+ 16 Zaidi ya hayo, msisahau kutenda mema na kushiriki vitu vyenu pamoja na wengine,+ kwa maana Mungu hupendezwa na dhabihu kama hizo.+

17 Watiini wale wanaoongoza kati yenu+ na mnyenyekee,+ kwa maana wanaendelea kuwalinda ninyi* kama wale watakaotoa hesabu,+ ili wafanye hivyo kwa shangwe na si kwa huzuni, kwa maana kufanya hivyo kungewadhuru ninyi.

18 Endeleeni kusali kwa ajili yetu, kwa maana tuna hakika kwamba tuna dhamiri nyoofu,* kwa kuwa tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.+ 19 Lakini hasa ninawahimiza ninyi msali kwamba nirudi kwenu haraka iwezekanavyo.

20 Basi Mungu wa amani, aliyemrudisha kutoka kwa wafu mchungaji mkuu+ wa kondoo, Bwana wetu Yesu, kwa damu ya agano linalodumu milele, 21 awape vifaa vyote vyema ili mfanye mapenzi yake, akitenda ndani yetu kupitia Yesu Kristo mambo yanayopendeza machoni pake, na awe na utukufu milele na milele. Amina.

22 Sasa ninawahimiza, akina ndugu, msikilize kwa subira neno hili la kutia moyo, kwa maana nimewaandikia barua fupi. 23 Ningependa kuwajulisha kwamba ndugu yetu Timotheo ameachiliwa huru. Akija hivi karibuni, nitakuja pamoja naye kuwaona.

24 Wapeni salamu zangu wote wanaoongoza kati yenu na watakatifu wote. Wale walio Italia+ wanawatumia salamu zao.

25 Fadhili zisizostahiliwa na ziwe pamoja nanyi nyote.

Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”

Au “wamwinamie.”

Au “watumishi wake wa watu wote.”

Au “haki.”

Au “utumishi wa watu wote.”

Au “miujiza.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “awakomboe.”

Tnn., “mbegu ya.”

Au “atoe dhabihu ya kufunika dhambi; kufunika dhambi.”

Au “mwaliko.”

Au “tunayemkiri.”

Yaani, Yesu.

Au “ushahidi.”

Au “tunakuwa na ushirika na.”

Tnn., “tuwe na woga.”

Angalia Kamusi.

Angalia Kamusi.

Au “zitusaidie wakati unaofaa.”

Au “kwa wororo; kwa kiasi.”

Au “wasiotii.”

Au “anakabiliana.”

Tnn., “Katika siku za mwili wake.”

Tnn., “kulingana na wakati.”

Au “nguvu zao za ufahamu.”

Angalia Kamusi.

Au “shauri.”

Au “aliingilia kati.” Tnn., “alifanya upatanisho.”

Au “ya uhai wetu.”

Tnn., “akamgawia.”

Au “kwa wakati wote.”

Au “mzee wa ukoo.”

Tnn., “wametoka katika kiuno cha.”

Tnn., “katika kiuno cha.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “hataghairi.”

Au “yule aliyewekwa kuwa rehani.”

Au “mtumishi wa watu wote.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “utumishi wa watu wote ulio bora.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “mikate ya wonyesho.”

Au “mahali pa kufunika dhambi.”

Tnn., “ubatizo wa aina mbalimbali.”

Tnn., “fidia ya; wokovu wa.”

Tnn., “halikuzinduliwa.”

Au “kitabu cha kukunjwa.”

Au “utumishi wa watu wote.”

Tnn., “mbele za uso wa.”

Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”

Au “hatakuja kushughulika na dhambi.”

Au labda, “watu hawawezi.”

Au “kufanya utumishi wa watu wote.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “uhakika.”

Tnn., “aliyotuzindulia.”

Au “tuhangaikiane.”

Au “kuhimizana.”

Angalia Nyongeza A5.

Tnn., “mlifunuliwa kama katika ukumbi wa maonyesho.”

Au “mliungana.”

Au “miliki.”

Tnn., “uhuru wenu wa kusema.”

Au “nafsi yangu haipendezwi.”

Au “nafsi zetu.”

Au “uthibitisho wenye kuridhisha.”

Au “mababu zetu.”

Au “vizazi.” Angalia Kamusi.

Au “alitoa ushahidi kwa kukubali.”

Au “yuko hai.”

Au “alimwogopa Mungu.”

Au “msanifu.”

Tnn., “mbegu.”

Au “anayetegemeka.”

Tnn., “mbegu.”

Yaani, kutoka katika nchi ya Misri.

Au “amri.”

Au “mazishi.”

Tnn., “asiwaguse.”

Au “vipandevipande.”

Angalia Kamusi.

Au “msizimie katika nafsi zenu.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “humwadhibu.”

Au “mazoezi.”

Tnn., “baba zetu wa mwili.”

Au “inahuzunisha.”

Tnn., “huzaa tunda lenye kufanya amani la uadilifu.”

Au “utakatifu.”

Angalia Kamusi, “Uasherati.”

Yaani, fikira za baba yake.

Tnn., “hakupata nafasi kwa ajili ya hilo.”

Au “msimpe visingizio: msimpuuze.”

Au “kuwaonyesha wageni fadhili; kuwa wakarimu.”

Tnn., “waliofungwa; walio katika vifungo.”

Au labda, “kana kwamba mnateseka pamoja nao.”

Angalia Kamusi, “Uasherati.”

Au “vya sasa.”

Angalia Nyongeza A5.

Yaani, sheria zinazohusu chakula.

Au “kuzilinda nafsi zenu.”

Tnn., “njema.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki