Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt Mhubiri 1:1-12:14
  • Mhubiri

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mhubiri
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Mhubiri

MHUBIRI

1 Maneno ya mkutanishaji,*+ mwana wa Daudi, mfalme wa Yerusalemu.+

 2 “Ubatili mkubwa kupita wote!” asema mkutanishaji,

“Ubatili mkubwa kupita wote! Kila kitu ni ubatili!”+

 3 Mtu hupata faida gani kutokana na kazi yake yote ngumu

Anayofanya kwa jasho chini ya jua?+

 4 Kizazi huenda, na kizazi huja,

Lakini dunia inadumu* milele.+

 5 Jua huchomoza,* na jua hutua;

Kisha hurudi haraka* mahali linapochomozea tena.+

 6 Upepo huelekea kusini na kuzungukazunguka hadi kaskazini;

Huendelea kuzungukazunguka; upepo huendelea na mizunguko yake.

 7 Vijito vyote* hutiririka kuingia baharini, lakini bado bahari haijai.+

Mahali vijito vinakotoka, huko ndiko vinakorudi ili vitiririke tena.+

 8 Mambo yote yanachosha sana;

Hakuna yeyote anayeweza hata kueleza jambo hilo.

Jicho halitosheki kuona;

Wala sikio halishibi kusikia.

 9 Jambo ambalo limekuwako, ndilo litakalokuwako,

Na jambo ambalo limefanywa, litafanywa tena;

Hakuna jambo jipya chini ya jua.+

10 Je, kuna jambo lolote ambalo mtu anaweza kusema, “Tazama jambo hili—ni jipya”?

Tayari lilikuwako tangu zamani za kale;

Lilikuwako kabla ya wakati wetu.

11 Hakuna yeyote anayewakumbuka watu wa zamani;

Wala hakuna yeyote atakayewakumbuka watakaokuja baadaye;

Wala hawatakumbukwa na wale watakaokuja hata baadaye.+

12 Mimi, mkutanishaji, nimekuwa mfalme wa Israeli huko Yerusalemu.+ 13 Niliazimia moyoni mwangu kujifunza na kuchunguza kwa hekima+ kila jambo ambalo limefanywa chini ya mbingu+—kazi ya kusikitisha ambayo Mungu amewapa wanadamu inayofanya waendelee kushughulika.

14 Niliona kazi zote zilizofanywa chini ya jua,

Na, tazama! kila jambo lilikuwa ubatili, kukimbiza upepo.+

15 Kilichopinda hakiwezi kunyooshwa,

Na kisichokuwapo huenda kisiweze kuhesabiwa.

16 Kisha nikasema moyoni mwangu: “Tazama! Nimepata hekima nyingi, kuliko mtu yeyote aliyenitangulia Yerusalemu,+ na moyo wangu ulipata hekima nyingi sana na ujuzi.”+ 17 Nilijitahidi sana ili moyo wangu ujue hekima na kujua wazimu* na kujua ujinga,+ na hilo pia ni kukimbiza upepo.

18 Kwa maana hekima nyingi humfanya mtu azidi kukata tamaa,

Hivi kwamba yeyote anayeongeza ujuzi anaongeza maumivu.+

2 Kisha nikasema moyoni mwangu: “Haya, acha nijaribu starehe,* nione ni jambo gani jema litakalokuja.” Lakini tazama! hilo pia lilikuwa ubatili.

 2 Nilisema hivi kuhusu kicheko: “Ni wazimu!”

Na kuhusu starehe,* “Ina faida gani?”

3 Nilijaribu kuufurahisha moyo wangu kwa divai,+ huku nikiendelea kuwa na hekima yangu; hata nilikumbatia ujinga ili nione jambo bora ambalo wanadamu wanapaswa kufanya katika siku chache wanazoishi chini ya mbingu. 4 Nilianza kufanya mambo makubwa.+ Nikajijengea nyumba;+ Nikajipandia mashamba ya mizabibu.+ 5 Nikajitengenezea mashamba na bustani, na humo nikapanda miti ya matunda ya kila aina. 6 Nikajichimbia mabwawa ya maji, ili kumwagilia maji msitu wenye miti iliyokuwa ikisitawi. 7 Nikapata watumishi wa kiume na wa kike,+ na watumishi wengine walizaliwa nyumbani mwangu.* Pia, nilipata mifugo mingi—ng’ombe na kondoo na mbuzi+—kuliko mtu yeyote aliyenitangulia Yerusalemu. 8 Nikajikusanyia fedha na dhahabu,+ hazina za* wafalme na za mikoa.+ Nikajikusanyia waimbaji wa kiume na wa kike, na pia chanzo cha raha tele kwa wanaume—mwanamke, naam, wanawake wengi. 9 Basi nikawa mkuu, nikamzidi mtu yeyote aliyenitangulia Yerusalemu.+ Nami nikaendelea kuwa na hekima yangu.

10 Sikujinyima chochote nilichotamani.*+ Sikuunyima moyo wangu raha* yoyote ile, kwa maana moyo wangu ulishangilia kwa sababu ya kazi yangu yote ngumu, na hiyo ndiyo iliyokuwa thawabu yangu* kwa sababu ya kazi yangu yote ngumu.+ 11 Lakini nilipofikiria kazi zote nilizofanya kwa mikono yangu mwenyewe na kazi yangu yote ngumu niliyofanya kwa jasho ili kuitimiza,+ niliona kwamba kila kitu kilikuwa ubatili, kukimbiza upepo;+ hakukuwa na kitu chochote chenye thamani ya kweli* chini ya jua.+

12 Basi nikaanza kuchunguza hekima na wazimu na ujinga.+ (Kwa maana mtu anayekuja baada ya mfalme anaweza kufanya nini? Anaweza kufanya tu jambo ambalo tayari limefanywa.) 13 Nami nikaona kwamba hekima ina faida kuliko ujinga,+ kama tu nuru ilivyo na faida kuliko giza.

14 Mtu mwenye hekima ana macho kichwani mwake;*+ lakini mpumbavu anatembea gizani.+ Pia nimegundua kwamba wote wana mwisho uleule. *+ 15 Kisha nikasema moyoni mwangu: “Kinachompata mpumbavu ndicho kitakachonipata mimi pia.”+ Sasa, basi, nilipata faida gani kwa kuwa na hekima kupita kiasi? Basi nikasema moyoni mwangu: “Hili pia ni ubatili.” 16 Kwa maana hakuna atakayekumbukwa daima, iwe ni mwenye hekima au mpumbavu.+ Siku zijazo, kila mtu atasahauliwa. Na mwenye hekima atakufa jinsi gani? Pamoja na mpumbavu.+

17 Basi nikachukia maisha,+ kwa sababu kila jambo linalofanywa chini ya jua lilionekana kwangu kuwa lenye kuhuzunisha, kwa sababu kila jambo lilikuwa ubatili,+ kukimbiza upepo.+ 18 Nikachukia vitu vyote nilivyokuwa nimefanya kazi ngumu chini ya jua ili kuvipata,+ kwa sababu ni lazima nimwachie mtu atakayekuja baada yangu.+ 19 Na ni nani anayejua ikiwa atakuwa mwenye hekima au mjinga?+ Lakini bado atamiliki vitu vyote nilivyotafuta kwa jitihada nyingi na hekima chini ya jua. Hilo pia ni ubatili. 20 Basi nikaanza kukata tamaa moyoni mwangu kwa sababu ya kazi yangu yote ngumu niliyofanya kwa jasho chini ya jua. 21 Kwa maana mtu anaweza kufanya kazi kwa bidii, akiongozwa na hekima na ujuzi na ustadi, lakini ni lazima amwachie fungu lake mtu ambaye hakulifanyia kazi.*+ Hili pia ni ubatili na ni msiba mkubwa.*

22 Kwa kweli mtu hupata faida gani kutokana na kazi yake yote ngumu na tamaa inayomchochea* kufanya kazi kwa bidii chini ya jua?+ 23 Kwa maana siku zake zote, kazi yake humletea maumivu na kumkatisha tamaa,+ na hata usiku moyo wake haupumziki.+ Hili pia ni ubatili.

24 Hakuna jambo bora analoweza kufanya mtu kuliko kula na kunywa na kufurahia* kazi yake ngumu.+ Hili pia nimegundua kwamba linatoka mkononi mwa Mungu wa kweli,+ 25 kwa maana ni nani anayekula na ni nani anayekunywa vizuri kuliko mimi?+

26 Yeye humpa mtu anayempendeza hekima na ujuzi na shangwe,+ lakini humpa mtenda dhambi kazi ya kukusanya na kurundika tu, ili ampe yule anayempendeza Mungu wa kweli.+ Hili pia ni ubatili, kukimbiza upepo.

3 Kuna wakati uliowekwa wa kila jambo,

Wakati wa kila shughuli chini ya mbingu:

 2 Wakati wa kuzaliwa na wakati wa kufa;

Wakati wa kupanda na wakati wa kung’oa kilichopandwa;

 3 Wakati wa kuua na wakati wa kuponya;

Wakati wa kubomoa na wakati wa kujenga;

 4 Wakati wa kulia na wakati wa kucheka;

Wakati wa kuomboleza kwa sauti na wakati wa kucheza dansi;*

 5 Wakati wa kutupa mawe na wakati wa kukusanya mawe;

Wakati wa kukumbatia na wakati wa kuacha kukumbatia;

 6 Wakati wa kutafuta na wakati wa kuacha kutafuta kilichopotea;

Wakati wa kuhifadhi na wakati wa kutupa;

 7 Wakati wa kurarua+ na wakati wa kushona,

Wakati wa kunyamaza+ na wakati wa kuongea;+

 8 Wakati wa kupenda na wakati wa kuchukia;+

Wakati wa vita na wakati wa amani.

9 Mfanyakazi hupata faida gani kutokana na jitihada zake zote?+ 10 Nimeona kazi ambayo Mungu amewapa wanadamu wajishughulishe nayo. 11 Amefanya kila kitu kipendeze* kwa wakati wake.+ Hata ameweka umilele katika moyo wao; lakini bado wanadamu hawatajua kamwe kazi ambayo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.

12 Nimefikia mkataa kwamba hakuna jambo bora wanaloweza kufanya kuliko kushangilia na kufanya mema maishani mwao,+ 13 na kwamba kila mtu anapaswa kula na kunywa na kufurahia kazi yake yote ngumu. Ni zawadi kutoka kwa Mungu.+

14 Sasa nimejua kwamba kazi zote za Mungu wa kweli zitadumu milele. Hakuna chochote kinachoweza kuongezwa wala chochote kinachoweza kupunguzwa kwenye kazi zake. Mungu wa kweli amezifanya ziwe hivyo, ili watu wamwogope.+

15 Jambo lolote linalotukia limewahi kutukia, na litakalokuja limewahi kuwepo;+ lakini Mungu wa kweli hutafuta kilichofuatiwa.*

16 Pia nimeona jambo hili chini ya jua: Badala ya haki kulikuwa na uovu, na badala ya uadilifu kulikuwa na uovu.+ 17 Basi nikasema moyoni mwangu: “Mungu wa kweli atawahukumu waadilifu na waovu,+ kwa maana kuna wakati kwa ajili ya kila kazi na kila tendo.”

18 Pia nikasema moyoni mwangu kwamba Mungu wa kweli atawajaribu wanadamu na kuwaonyesha kwamba wao ni kama wanyama, 19 kwa maana kuna mwisho wa* wanadamu na mwisho wa wanyama; wote wana mwisho uleule.+ Anavyokufa huyu, ndivyo anavyokufa huyu; na wote wana roho ileile.+ Kwa hiyo mwanadamu si bora kuliko wanyama, kwa maana kila kitu ni ubatili. 20 Wote wanaenda mahali palepale.+ Wote wanatoka mavumbini,+ na wote wanarudi mavumbini.+ 21 Kwa kweli ni nani anayejua ikiwa roho ya wanadamu hupanda kwenda juu, na ikiwa roho ya wanyama hushuka chini ardhini?+ 22 Nami nikaona kwamba hakuna jambo bora kwa mwanadamu kuliko kufurahia kazi yake,+ kwa sababu hiyo ndiyo zawadi yake;* kwa maana ni nani anayeweza kumwezesha aone yatakayotukia baada ya kifo chake?+

4 Tena, nikakazia uangalifu matendo yote ya ukandamizaji yanayofanywa chini ya jua. Nikaona machozi ya wanaokandamizwa, na hakukuwa na mtu yeyote wa kuwafariji.+ Na wale waliowakandamiza walikuwa na nguvu, lakini waliokandamizwa hawakuwa na mtu yeyote wa kuwafariji. 2 Nami nikawapongeza wafu ambao tayari walikuwa wamekufa badala ya walio hai ambao bado walikuwa hai.+ 3 Na yule ambaye hajazaliwa ni afadhali kuliko hao wawili,+ kwa kuwa hajaona mambo yenye kuhuzunisha yanayofanywa chini ya jua.+

4 Nami nimeona jinsi ambavyo ushindani kati ya watu unavyowafanya wajitahidi sana* na kufanya kazi kwa ustadi;+ hili pia ni ubatili, kukimbiza upepo.

5 Mpumbavu hukunja mikono yake huku mwili wake ukiendelea kudhoofika.*+

6 Ni afadhali konzi moja ya pumziko kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kukimbiza upepo.+

7 Nilikazia uangalifu mfano mwingine wa ubatili chini ya jua: 8 Kuna mtu aliye peke yake, asiye na rafiki yeyote; hana mwana wala ndugu, lakini kazi yake yote ngumu haina mwisho. Macho yake hayatosheki kamwe na utajiri.+ Lakini je, yeye hujiuliza, ‘Ninafanya kazi kwa bidii na kujinyima* vitu vyema kwa ajili ya nani’?+ Hili pia ni ubatili na ni kazi inayosikitisha.+

9 Wawili ni afadhali kuliko mmoja+ kwa sababu wanapata thawabu njema* kwa kazi yao ngumu. 10 Kwa maana mmoja wao akianguka, mwenzake anaweza kumwinua. Lakini itakuwaje kwa yule atakayeanguka naye hana mtu wa kumwinua?

11 Tena, wawili wakilala pamoja, watapata joto, lakini mtu mmoja tu atapataje joto? 12 Na mtu anaweza kumzidi nguvu aliye peke yake, lakini wawili walio pamoja wanaweza kukabiliana naye. Na kamba ya nyuzi tatu haikatiki upesi.*

13 Ni afadhali mtoto maskini lakini mwenye hekima kuliko mfalme mzee lakini mpumbavu,+ ambaye hana tena ufahamu wa kutosha wa kutii onyo.+ 14 Kwa maana alitoka* gerezani ili awe mfalme,+ ingawa alizaliwa maskini katika utawala wa mfalme huyo.+ 15 Niliwafikiria wote walio hai wanaotembeatembea chini ya jua, na pia hali ya yule mtawala kijana anayechukua mahali pa yule mfalme. 16 Ingawa idadi ya wafuasi wake wote haina mwisho, wale watakaokuja baadaye hawatafurahishwa naye.+ Hili pia ni ubatili, kukimbiza upepo.

5 Uwe mwangalifu* wakati wowote unapoenda katika nyumba ya Mungu wa kweli;+ ni afadhali ukaribie ili kusikiliza+ badala ya kutoa dhabihu kama wanavyofanya wapumbavu,+ kwa maana hawajui kwamba jambo wanalofanya ni baya.

2 Usifungue kinywa chako haraka, wala usiruhusu moyo wako uzungumze bila kufikiri mbele za Mungu wa kweli,+ kwa maana Mungu wa kweli yuko mbinguni lakini wewe uko duniani. Ndiyo sababu maneno yako yanapaswa kuwa machache.+ 3 Kwa maana ndoto huja kwa sababu ya shughuli nyingi sana,*+ na mpumbavu huropoka kwa sababu ya kuwa na maneno mengi sana.+ 4 Wakati wowote unapoweka nadhiri kwa Mungu,+ usikawie kuitimiza, kwa maana hapendezwi na wapumbavu.+ Unapoweka nadhiri, itimize.+ 5 Ni afadhali usiweke nadhiri kuliko kuweka nadhiri na kukosa kuitimiza.+ 6 Usiruhusu kinywa chako kikufanye* utende dhambi,+ wala usiseme mbele ya malaika* kwamba nilikosea.+ Kwa nini umkasirishe Mungu wa kweli kwa yale unayosema hivi kwamba alazimike kuiharibu kazi ya mikono yako?+ 7 Kwa maana kama vile shughuli nyingi zinavyomfanya mtu aote ndoto,+ vivyo hivyo, maneno mengi huongoza kwenye ubatili. Lakini mwogope Mungu wa kweli.+

8 Ukiona maskini wakikandamizwa kwa njia yoyote ile na haki na uadilifu zikikiukwa katika wilaya yenu, usishangazwe na jambo hilo.+ Kwa maana ofisa huyo mkuu anatazamwa na yule aliye juu zaidi yake, na kuna wengine walio juu zaidi yao.

9 Pia, faida ya nchi hugawanywa miongoni mwao wote; hata mfalme huhudumiwa kutokana na shamba hilo.+

10 Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato.+ Hili pia ni ubatili.+

11 Vitu vizuri vinapoongezeka, walaji huongezeka.+ Na mwenye vitu hivyo hupata faida gani, ila kuviangalia tu kwa macho yake?+

12 Usingizi wa mtumishi ni mtamu, iwe anakula kidogo au kingi, lakini wingi alionao tajiri haumruhusu kulala usingizi.

13 Kuna msiba mkubwa ambao* nimeona chini ya jua: utajiri uliorundikwa na mtu na kumdhuru yeye mwenyewe. 14 Utajiri huo ulipotea kwa sababu ya mradi ambao haukufanikiwa,* na anapomzaa mwana, habaki na kitu chochote.+

15 Kama mtu alivyotoka katika tumbo la mama yake akiwa uchi, ndivyo atakavyoenda, kama alivyokuja.+ Naye hawezi kwenda na chochote alichopata kutokana na kazi yake yote ngumu.+

16 Huu pia ni msiba mkubwa:* Kama tu alivyokuja, ndivyo atakavyoenda; na mtu ambaye anafanya kazi kwa bidii daima kwa ajili ya upepo anapata faida gani?+ 17 Pia, yeye hula gizani kila siku, akiwa amekata tamaa kabisa na akiwa mgonjwa na akiwa amekasirika kabisa.+

18 Hili ndilo jambo ambalo nimeona ni jema na linafaa: kwamba mtu anapaswa kula na kunywa na kufurahia kazi yote ngumu+ anayofanya kwa jasho chini ya jua katika siku chache za maisha alizopewa na Mungu wa kweli, kwa maana hiyo ndiyo thawabu yake.*+ 19 Pia, Mungu wa kweli anapompa mtu utajiri na mali+ pamoja na uwezo wa kufurahia vitu hivyo, anapaswa kuchukua thawabu yake* na kushangilia katika kazi yake ngumu. Hiyo ndiyo zawadi kutoka kwa Mungu.+ 20 Kwa maana hataona* kwa urahisi jinsi siku za maisha yake zinavyopita, kwa sababu Mungu wa kweli humshughulisha na shangwe ya moyo wake.+

6 Kuna msiba mwingine* ambao nimeona chini ya jua, nao ni wa kawaida miongoni mwa wanadamu: 2 Mungu wa kweli humpa mtu utajiri na mali na utukufu, hivi kwamba hakosi chochote anachotamani;* lakini Mungu wa kweli hamwezeshi kuvifurahia, ingawa mgeni anaweza kuvifurahia. Hili ni ubatili na ni mateso makali. 3 Mtu akizaa watoto mia moja, aishi miaka mingi na kuzeeka, lakini hafurahii vitu vyake vizuri kabla hajaingia kaburini, sina budi kusema kwamba mtoto aliyefia tumboni ni afadhali kuliko mtu huyo.+ 4 Kwa maana mtoto huyo alikuja bure na kwenda zake gizani, na jina lake limetokomea gizani. 5 Hata ingawa hakuwahi kuliona jua wala kujua kitu chochote, yeye bado ni afadhali* kuliko mtu huyo.+ 6 Kuna faida gani ya kuishi miaka elfu moja mara mbili lakini bila furaha? Je, wote hawaendi mahali palepale?+

7 Kazi yote ngumu ambayo mtu hufanya ni kwa ajili ya kujaza kinywa chake;+ na bado hamu* yake haitoshelezwi kamwe. 8 Kwa maana mwenye hekima anamzidi mpumbavu kwa njia gani,+ au maskini hupata faida gani akijua jinsi ya kukabiliana na maisha?* 9 Ni afadhali mtu afurahie mambo ambayo macho yanaona kuliko kutangatanga akifuatia tamaa zake.* Hili pia ni ubatili, kukimbiza upepo.

10 Chochote ambacho kimekuwapo, tayari kimepewa jina, na mwanadamu anajulikana alivyo; naye hawezi kuzozana na* yule aliye na nguvu zaidi yake. 11 Kadiri maneno* yalivyo mengi, ndivyo ubatili ulivyo mwingi; nayo humnufaishaje mwanadamu? 12 Ni nani anayejua ni jambo gani lililo bora kwa mwanadamu kufanya maishani katika siku chache za maisha yake ya ubatili, anazotumia kama kivuli?+ Kwa maana ni nani anayeweza kumwambia mwanadamu yatakayotukia chini ya jua baada ya kifo chake?

7 Jina zuri* ni bora kuliko mafuta mazuri,+ na siku ya kufa ni bora kuliko siku ya kuzaliwa. 2 Ni afadhali kwenda katika nyumba yenye maombolezo kuliko kwenda katika nyumba yenye karamu,+ kwa sababu huo ndio mwisho wa kila mwanadamu, na walio hai wanapaswa kuweka moyoni jambo hilo. 3 Ni afadhali huzuni kuliko kicheko,+ kwa maana uso wenye huzuni huboresha moyo.+ 4 Moyo wa mwenye hekima uko katika nyumba yenye maombolezo, lakini moyo wa mpumbavu uko katika nyumba yenye nderemo.*+

5 Ni afadhali kusikiliza karipio la mtu mwenye hekima+ kuliko kusikiliza wimbo wa wajinga. 6 Kwa maana kicheko cha mjinga ni kama mlio wa miiba inayoteketea chini ya chungu;+ na hili pia ni ubatili. 7 Lakini ukandamizaji unaweza kumfanya mtu mwenye hekima ashikwe na wazimu, na rushwa huupotosha moyo.+

8 Ni afadhali mwisho wa jambo kuliko mwanzo wake. Ni bora kuwa na subira kuliko kuwa na roho ya kiburi.+ 9 Usikasirike haraka,*+ kwa maana hasira hukaa katika kifua cha wajinga.*+

10 Usiulize: “Mbona siku za zamani zilikuwa bora kuliko hizi?” kwa maana hukuuliza hivyo kwa hekima.+

11 Hekima pamoja na urithi ni jambo jema na huwanufaisha wale wanaoona mwanga wa mchana.* 12 Kwa maana hekima ni ulinzi+ kama pesa zilivyo ulinzi,+ lakini hii ndiyo faida ya ujuzi: Hekima humhifadhi hai yule aliye nayo.+

13 Tafakari kazi ya Mungu wa kweli, kwa maana ni nani anayeweza kunyoosha kitu ambacho amekipinda?+ 14 Siku iliyo njema, tafakari wema huu,+ lakini katika siku ya taabu,* zingatia kwamba Mungu ameifanya hii na hiyo nyingine,+ ili wanadamu wasiweze kuwa na uhakika kuhusu* jambo lolote litakalowapata wakati ujao.+

15 Katika maisha yangu ya ubatili+ nimeona kila jambo—nimemwona mwadilifu akiangamia katika uadilifu wake+ na mwovu akiishi maisha marefu licha ya uovu wake.+

16 Usiwe mwadilifu kupita kiasi,+ wala kujifanya mwenye hekima kupita kiasi.+ Kwa nini ujiangamize?+ 17 Usiwe mwovu kupita kiasi, wala kuwa mjinga.+ Kwa nini ufe kabla ya wakati wako?+ 18 Ni bora kushika kabisa onyo moja bila kuachilia lingine;+ kwa maana anayemwogopa Mungu atatii yote mawili.

19 Hekima humfanya mtu mwenye hekima awe na nguvu zaidi kuliko wanaume kumi wenye nguvu walio jijini.+ 20 Kwa maana hakuna mtu mwadilifu duniani anayefanya mema sikuzote na hatendi dhambi kamwe.+

21 Pia, usitie moyoni kila neno linalosemwa na watu;+ la sivyo, huenda ukamsikia mtumishi wako akisema mambo maovu kukuhusu;* 22 kwa maana unajua vema moyoni mwako kwamba wewe mwenyewe umesema mambo maovu kuwahusu wengine.+

23 Niliyapima mambo hayo yote kwa hekima, nikasema: “Nitakuwa na hekima.” Lakini ilikuwa mbali nami. 24 Lile ambalo limekuja kuwapo halifikiki nalo ni lenye kina kirefu sana. Ni nani anayeweza kulielewa?+ 25 Niliuongoza moyo wangu kujua na kuchunguza na kutafuta hekima na maana ya mambo, na kuelewa uovu wa upumbavu na ujinga wa kuwa wazimu.+ 26 Kisha nikagundua hili: Mwanamke ambaye ni kama wavu wa mwindaji anatia uchungu kuliko kifo, ambaye moyo wake ni kama nyavu za kukokotwa, na ambaye mikono yake ni kama minyororo ya gereza. Mtu anayempendeza Mungu wa kweli atamkwepa mwanamke huyo,+ lakini mtenda dhambi hunaswa naye.+

27 “Tazama, hili ndilo nililogundua,” asema mkutanishaji.+ “Nilichunguza jambo moja baada ya lingine ili nifikie mkataa wangu, 28 lakini jambo nililoendelea* kutafuta, sijalipata. Nimempata mwanamume mmoja* kati ya elfu moja, lakini sijampata mwanamke miongoni mwao. 29 Hili ndilo jambo pekee nililopata: Mungu wa kweli aliwaumba wanadamu wakiwa wanyoofu,+ lakini wao wenyewe wamejitafutia mipango mingi.”+

8 Ni nani aliye kama mwenye hekima? Ni nani anayejua suluhisho la tatizo?* Hekima ya mtu huutia nuru uso wake na kuilainisha sura yake ngumu.

2 Nasema: “Tii maagizo ya mfalme+ kwa sababu ya kiapo chako kwa Mungu.+ 3 Usifanye haraka kuondoka mbele ya mfalme.+ Usitetee jambo lolote baya;+ kwa kuwa anaweza kufanya jambo lolote apendalo, 4 kwa sababu neno la mfalme ni uamuzi wa mwisho;+ ni nani anayeweza kumuuliza: ‘Unafanya nini?’”

5 Mtu anayeshika amri hatapata madhara,+ na moyo wenye hekima utajua wakati unaofaa na utaratibu unaofaa.*+ 6 Kwa maana kila jambo lina wakati wake na utaratibu wake,*+ kwa sababu matatizo ya wanadamu ni mengi sana. 7 Kwa kuwa hakuna mtu anayejua litakalotukia, ni nani anayeweza kumwambia jinsi litakavyotukia?

8 Kama vile ambavyo hakuna mtu aliye na nguvu juu ya roho* au anayeweza kuizuia roho, vivyo hivyo hakuna yeyote aliye na nguvu juu ya siku ya kufa.+ Kama vile ambavyo hakuna yeyote anayeruhusiwa kurudi nyumbani wakati wa vita, vivyo hivyo uovu hautawaruhusu wale wanaozoea kuutenda waponyoke.*

9 Hayo yote nimeyaona, nami nimetafakari moyoni mwangu kila kazi ambayo imefanywa chini ya jua, wakati ambapo mwanadamu amemtawala mwanadamu mwenzake kwa kumuumiza.*+ 10 Nami nikaona waovu wakizikwa, wale waliokuwa wakiingia na kutoka mahali patakatifu, lakini walisahauliwa upesi katika jiji ambalo walitenda hivyo.+ Hili pia ni ubatili.

11 Kwa sababu hukumu dhidi ya tendo ovu haijatekelezwa upesi,+ moyo wa wanadamu hupata ujasiri wa kutenda uovu.+ 12 Ingawa huenda mwovu akatenda uovu mara mia moja na bado aishi kwa muda mrefu, hata hivyo ninajua kwamba mambo yatawaendea vyema wale wanaomwogopa Mungu wa kweli, kwa sababu wanamwogopa.+ 13 Lakini mambo hayatamwendea vyema mwovu,+ wala hatarefusha siku zake zilizo kama kivuli,+ kwa sababu hamwogopi Mungu.

14 Kuna jambo la ubatili* ambalo hutukia duniani: Kuna watu waadilifu wanaotendewa kana kwamba walikuwa wametenda uovu,+ na kuna watu waovu wanaotendewa kana kwamba walikuwa wametenda uadilifu.+ Nasema kwamba hili pia ni ubatili.

15 Basi nikapendekeza kushangilia,+ kwa sababu hakuna jambo bora kwa mwanadamu chini ya jua kuliko kula na kunywa na kushangilia; mambo hayo yanapaswa kufuatana naye anapofanya kazi kwa bidii sikuzote za maisha yake,+ ambazo Mungu wa kweli anampa chini ya jua.

16 Nilijitahidi sana ili moyo wangu upate hekima na ili nione shughuli* zote zinazofanywa duniani,+ hata nilikosa usingizi usiku na mchana.* 17 Kisha nikatafakari kazi yote ya Mungu wa kweli, nikatambua kwamba wanadamu hawawezi kufahamu kinachotukia chini ya jua.+ Hata wanadamu wakijitahidi kadiri gani, hawawezi kuifahamu. Hata wakidai kwamba wana hekima ya kutosha kujua, kwa kweli hawawezi kuifahamu.+

9 Kwa hiyo nikatia moyoni mambo hayo yote na kufikia mkataa wa kwamba waadilifu na wenye hekima, na pia kazi zao, zimo mikononi mwa Mungu wa kweli.+ Wanadamu hawajui upendo na chuki iliyokuwepo kabla yao. 2 Wote huwa na mwisho uleule,*+ waadilifu na waovu,+ watu wema na safi na wale wasio safi, wale wanaotoa dhabihu na wale wasiotoa dhabihu. Mtu mwema ni sawa na mtenda dhambi; mtu anayeapa ni sawa na yule anayejihadhari kuhusu kuapa. 3 Jambo hili linalohuzunisha hutukia chini ya jua: Kwa kuwa wote wana mwisho uleule,*+ moyo wa wanadamu umejaa pia uovu; na kuna wazimu moyoni mwao muda wote wa maisha yao, kisha wanakufa!*

4 Kuna tumaini kwa yeyote aliye miongoni mwa walio hai, kwa sababu mbwa aliye hai ni afadhali kuliko simba aliyekufa.+ 5 Kwa maana walio hai wanajua* kwamba watakufa,+ lakini waliokufa hawajui jambo lolote kamwe,+ wala hawana thawabu* tena, kwa sababu kumbukumbu lote kuwahusu limesahauliwa.+ 6 Pia, upendo wao na chuki yao na wivu wao tayari umetoweka, na hawana tena fungu lolote katika mambo yanayofanywa chini ya jua.+

7 Nenda, ule chakula chako kwa shangwe, na unywe divai yako kwa moyo mchangamfu,+ kwa kuwa tayari Mungu wa kweli amefurahia kazi zako.+ 8 Mavazi yako na yawe meupe daima,* na usikose kupaka kichwa chako mafuta.+ 9 Furahia maisha pamoja na mke wako mpendwa+ sikuzote za maisha yako ya ubatili, ambazo Mungu amekupa chini ya jua, sikuzote za ubatili wako, kwa maana hilo ndilo fungu lako maishani na katika kazi yako ngumu unayofanya kwa jasho chini ya jua.+ 10 Jambo lolote unalofanya kwa mkono wako, lifanye kwa nguvu zako zote, kwa sababu hakuna kazi wala mipango wala ujuzi wala hekima Kaburini,*+ mahali unapokwenda.

11 Nimeona jambo lingine chini ya jua, ya kwamba sikuzote si wenye mbio wanaoshinda mbio, wala wenye nguvu hawashindi vita,+ wala wenye hekima hawapati chakula sikuzote, wala werevu hawawi na utajiri sikuzote,+ wala wenye ujuzi hawafanikiwi sikuzote,+ kwa sababu wakati na matukio yasiyotarajiwa* huwapata wote. 12 Kwa maana mwanadamu hajui wakati wake.+ Kama samaki wanavyonaswa na wavu mwovu na ndege wanavyonaswa na mtego, ndivyo wanadamu wanavyonaswa wakati wa msiba, unapowapata kwa ghafla.

13 Niliona pia jambo hili kuhusu hekima chini ya jua—nalo likanivutia: 14 Kulikuwa na jiji dogo lenye wanaume wachache; na mfalme mwenye nguvu akaja, akalizingira, na kujenga ukuta mkubwa ili kulishambulia. 15 Mtu fulani maskini lakini mwenye hekima alipatikana katika jiji hilo, naye akaliokoa kwa hekima yake. Lakini hakuna aliyemkumbuka maskini huyo.+ 16 Basi nikajiambia: ‘Hekima ni bora kuliko nguvu;+ hata hivyo hekima ya maskini hudharauliwa, na maneno yake hayasikilizwi.’+

17 Ni afadhali kusikiliza maneno matulivu ya wenye hekima kuliko kelele za yule anayetawala miongoni mwa wajinga.

18 Hekima ni bora kuliko silaha za vita, lakini mtenda dhambi mmoja tu anaweza kuharibu mambo mengi mazuri.+

10 Kama nzi waliokufa wanavyofanya mafuta ya mtengenezaji wa marashi yanuke na kutoa povu, ndivyo ujinga kidogo unavyozidi hekima na utukufu.+

2 Moyo wa mwenye hekima humwongoza katika njia inayofaa,* lakini moyo wa mpumbavu humwongoza katika njia isiyofaa.*+ 3 Katika njia yoyote ambayo mjinga anatembea, hana busara,*+ naye huacha kila mtu ajue kwamba yeye ni mjinga.+

4 Hasira* ya mtawala ikiwaka dhidi yako, usiondoke mahali pako,+ kwa maana utulivu huzuia dhambi kubwa.+

5 Kuna jambo linalohuzunisha ambalo nimeona chini ya jua, aina ya kosa linalofanywa na watawala:+ 6 Ujinga huwekwa katika vyeo vingi vya juu, lakini matajiri* hubaki kwenye vyeo vya chini.

7 Nimeona watumishi wakiwa wamepanda farasi lakini wakuu wakitembea kwa miguu kama watumishi tu.+

8 Anayechimba shimo huenda akaanguka ndani yake;+ na anayebomoa ukuta wa mawe huenda akaumwa na nyoka.

9 Anayechimbua mawe huenda yakamuumiza, na yule anayepasua magogo huenda yakamuumiza.*

10 Ikiwa kifaa cha chuma hakina makali na mtu hakinoi, atahitaji kutumia nguvu nyingi. Lakini hekima husaidia kuleta mafanikio.

11 Nyoka akiuma kabla hajachezeshwa, mtu anayemchezesha kwa ustadi* hapati faida yoyote.

12 Maneno yanayotoka kwenye kinywa cha mwenye hekima huleta kibali,+ lakini midomo ya mpumbavu ndiyo inayomwangamiza.+ 13 Maneno ya kwanza yanayotoka katika kinywa chake ni ujinga,+ na maneno yake ya mwisho ni wazimu unaoleta msiba. 14 Lakini mjinga huendelea kuongea.+

Mwanadamu hajui yatakayotukia; ni nani anayeweza kumwambia yatakayotukia baada yake?+

15 Kazi ngumu ya mpumbavu humchosha kabisa, kwa sababu hata hajui jinsi atakavyofika jijini.

16 Ole kwa nchi ambayo mfalme wake ni mvulana+ na wakuu wake huanza karamu asubuhi! 17 Yenye furaha ni nchi ambayo mfalme wake ni mwana wa watu mashuhuri na wakuu wake hula wakati unaofaa ili wapate nguvu, si walewe!+

18 Kwa sababu ya uvivu unaopita kiasi paa hubonyea, na kwa sababu ya mikono milegevu nyumba huvuja.+

19 Mkate umekusudiwa* kuleta kicheko, na divai hufanya maisha yafurahishe;+ lakini pesa ni jawabu la mahitaji yote.+

20 Usimtukane* mfalme hata katika mawazo yako,*+ na usiwatukane matajiri katika chumba chako cha kulala; kwa sababu huenda ndege* akapeleka habari zako,* au huenda kiumbe mwenye mabawa akarudia lililosemwa.

11 Tupa* mkate wako juu ya maji,+ kwa maana baada ya siku nyingi utaupata tena.+ 2 Wagawie watu saba au hata wanane,+ kwa maana hujui ni msiba gani utakaotokea* duniani.

3 Mawingu yakijaa maji, mvua itanyesha duniani; na mti ukianguka kuelekea kusini au kaskazini, utabaki mahali ulipoanguka.

4 Anayeangalia upepo hatapanda mbegu, na anayetazama mawingu hatavuna.+

5 Kama usivyojua jinsi roho inavyofanya kazi ndani ya mifupa ya mtoto aliye tumboni mwa mama yake,+ vivyo hivyo hujui kazi ya Mungu wa kweli, anayefanya mambo yote.+

6 Panda mbegu zako asubuhi na usipumzishe mkono wako mpaka jioni;+ kwa maana hujui ni mbegu gani itakayofanikiwa, hii au ile, au ikiwa zote mbili zitafanikiwa.

7 Mwangaza ni mtamu, na ni vizuri macho yaone jua. 8 Kwa maana ikiwa mwanadamu ataishi miaka mingi, na aifurahie yote.+ Lakini anapaswa kukumbuka kwamba huenda siku za giza zikawa nyingi; yote yatakayokuja ni ubatili.+

9 Shangilia, ewe kijana, wakati ungali kijana, na moyo wako ushangilie siku za ujana wako. Fuata njia za moyo wako na uende mahali ambapo macho yako yanakuongoza; lakini ujue kwamba Mungu wa kweli atakuhukumu* kwa sababu ya mambo hayo yote.+ 10 Kwa hiyo ondoa mahangaiko moyoni mwako, na ujiepushe na mambo yanayodhuru mwili wako, kwa maana ujana na upeo wa maisha ni ubatili.+

12 Basi, mkumbuke Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako,+ kabla hazijaja siku za taabu*+ wala haijafika miaka utakaposema: “Siifurahii”; 2 kabla jua na mwangaza na mwezi na nyota hazijawa na giza,+ na mawingu kurudi baada ya* mvua kubwa; 3 siku ambayo walinzi* wa nyumba wanatetemeka,* na wanaume wenye nguvu wanainama, na wanawake wanaacha kusaga kwa sababu wamekuwa wachache, na mabibi wanaochungulia madirishani wanaona giza;+ 4 milango inayoelekea barabarani inapokuwa imefungwa, sauti ya jiwe la kusagia inapopungua, mtu anapoamshwa na mlio wa ndege, na mabinti wote wanaoimba wanapofifia.+ 5 Pia, mtu anapoogopa sehemu zilizo juu, na vitisho vinapokuwa barabarani. Na mti wa mlozi unapochanua,+ na panzi anapojikokota, na pilipili inapopasuka, kwa sababu mwanadamu anatembea kwenda kwenye nyumba yake ya kudumu+ na waombolezaji wanatembeatembea barabarani;+ 6 kabla kamba ya fedha haijaondolewa, na bakuli la dhahabu kuvunjwa, na mtungi ulio kwenye chemchemi kuvunjika, na gurudumu la tangi la maji kuvunjwa. 7 Kisha mavumbi hurudi ardhini,+ mahali yalikotoka, na roho* hurudi kwa Mungu wa kweli aliyewapa wanadamu.+

8 “Ubatili mkubwa kupita wote!” asema mkutanishaji.+ “Kila kitu ni ubatili.”+

9 Mkutanishaji hakupata tu hekima bali pia aliendelea kuwafundisha watu mambo aliyojua,+ naye alitafakari na kufanya uchunguzi kamili ili atunge* methali nyingi.+⁠ 10 Mkutanishaji alijitahidi kutafuta maneno yanayopendeza+ na kuandika maneno sahihi ya kweli.

11 Maneno ya wenye hekima ni kama michokoo ya kuongozea ng’ombe,+ na misemo yao iliyokusanywa ni kama misumari iliyopigiliwa ikawa imara; yametolewa na mchungaji mmoja. 12 Kuhusu jambo lingine lolote zaidi ya hayo, mwanangu, jihadhari: Hakuna mwisho wa kutunga vitabu vingi, na kuvisoma sana huuchosha sana mwili.+

13 Huu ndio umalizio, baada ya mambo yote kusikiwa: Mwogope Mungu wa kweli+ na ushike amri zake,+ kwa maana huu ndio wajibu wote wa mwanadamu.+ 14 Kwa maana Mungu wa kweli atahukumu kila tendo, kutia ndani kila jambo lililofichwa, kuwa jema au baya.+

Au “yule anayewakusanya watu; mhubiri.”

Tnn., “inasimama.”

Au “huangaza.”

Au “hurudi likihemahema.”

Au “Vijito vyote vya majira ya baridi kali; Vijito vyote vya majira.”

Au “upumbavu wa kupindukia.”

Au “kushangilia.”

Yaani, kushangilia.

Tnn., “na nilikuwa na wana wa nyumba.”

Au “mali ambazo kwa kawaida ni za.”

Tnn., “ambacho macho yangu yaliomba.”

Au “shangwe.”

Au “na hilo ndilo lililokuwa fungu langu.”

Au “manufaa.”

Au “anafungua macho yake.”

Au “hatima ileile.”

Au “ampe vitu vyote mtu ambaye hakuvifanyia kazi.”

Au “janga kubwa.”

Tnn., “jitihada za moyo wake za.”

Au “kuifanya nafsi yake ione mema kwa sababu ya.”

Tnn., “kuruka; kurukaruka.”

Au “kiwe na mpangilio mzuri; kifae.”

Au labda, “kilichopitilia mbali.”

Au “hatima ya.”

Au “hilo ndilo fungu lake.”

Au “wajitahidi kufanya kazi ya jasho.”

Tnn., “naye anakula mwili wake mwenyewe.”

Au “kuinyima nafsi yangu.”

Au “faida kubwa zaidi.”

Au “kwa urahisi.”

Labda ni yule mtoto mwenye hekima.

Au “Chunga hatua zako.”

Au “mahangaiko mengi sana.”

Tnn., “mwili wako ukufanye.”

Au “mjumbe.”

Au “janga kubwa ambalo.”

Tnn., “kazi ya msiba.”

Au “Hili pia ni janga kubwa.”

Au “hilo ndilo fungu lake.”

Au “fungu lake.”

Au “hatakumbuka.”

Au “janga lingine.”

Au “hakosi chochote kwa ajili ya nafsi yake.”

Tnn., “ana pumziko zaidi.”

Au “nafsi.”

Tnn., “kutembea mbele ya walio hai.”

Tnn., “kutangatanga kwa nafsi.”

Au “kujitetea mbele ya.”

Au labda, “mambo.”

Au “Sifa nzuri.” Tnn., “Kuwa na jina.”

Au “burudani.”

Tnn., “Usiwe mwepesi kukasirika rohoni mwako.”

Au labda, “ni dalili ya mjinga.”

Yaani, walio hai.

Au “majanga.”

Au “kugundua.”

Tnn., “akikulaani.”

Au “ambalo nafsi yangu iliendelea.”

Au “mwanamume mmoja mnyoofu.”

Au “maana ya jambo.”

Au “hukumu inayofaa.”

Au “hukumu yake.”

Au “pumzi, upepo.”

Au labda, “uovu hauwezi kuwaokoa waovu.”

Au “kumdhuru; kumletea hasara.”

Au “linalovunja moyo.”

Au “kazi.”

Au labda, “kwamba watu hawalali mchana wala usiku.”

Au “hatima ileile.”

Au “hatima ileile.”

Tnn., “baada ya hilo wanaenda kwa waliokufa!”

Au “wanatambua.”

Au “malipo.”

Yaani, mavazi yanayong’aa yanayoashiria uchangamfu, si mavazi ya maombolezo.

Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.

Au “tukio lisilotazamiwa.”

Tnn., “uko kwenye mkono wake wa kulia.”

Tnn., “uko kwenye mkono wake wa kushoto.”

Tnn., “moyo wake umepungukiwa.”

Tnn., “Roho, Pumzi.”

Au “wanaostahili.”

Au labda, “anapaswa kujihadhari nayo.”

Tnn., “stadi wa ulimi.”

Au “Chakula kimekusudiwa.”

Au “Usimlaani.”

Au labda, “kitandani mwako.”

Tnn., “kiumbe anayeruka angani.”

Tnn., “sauti yako.”

Au “Sambaza.”

Au “janga gani litakalotokea.”

Au “atakufanya uwajibike.”

Au “msiba.”

Au labda, “yakiwa na.”

Au “watunzaji.”

Au “wanatikisika.”

Au “nguvu ya uhai.”

Au “apange kwa utaratibu.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki