KWA WAROMA
1 Paulo, mtumwa wa Kristo Yesu aliyeitwa awe mtume na kuwekwa kando kwa ajili ya habari njema ya Mungu,+ 2 ambayo aliahidi mapema kupitia manabii wake katika Maandiko matakatifu, 3 kuhusu Mwana wake, aliyetokana na uzao wa* Daudi+ kulingana na mwili, 4 lakini ambaye kwa nguvu alitangazwa kuwa Mwana wa Mungu+ kulingana na roho ya utakatifu kupitia ufufuo kutoka kwa wafu+—ndiyo, Yesu Kristo Bwana wetu. 5 Kupitia yeye tulipokea fadhili zisizostahiliwa na utume+ ili watu wa mataifa yote+ wamtii na kuwa na imani na kulitukuza jina lake, 6 ninyi pia mmeitwa kutoka kwa mataifa hayo ili muwe wa Yesu Kristo— 7 kwa ninyi nyote mlio huko Roma mkiwa wapendwa wa Mungu, walioitwa wawe watakatifu:
Na muwe na fadhili zisizostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo.
8 Kwanza kabisa, ninamshukuru Mungu wangu kupitia Yesu Kristo kuwahusu ninyi nyote, kwa sababu imani yenu inazungumzwa ulimwenguni kote. 9 Kwa maana Mungu, ambaye ninamtolea utumishi mtakatifu kwa roho yangu kuhusiana na ile habari njema kuhusu Mwana wake, ni shahidi wangu wa jinsi ninavyowataja sikuzote katika sala zangu bila kuacha,+ 10 nikiomba kwamba ikiwezekana, hatimaye nifanikiwe kuja kwenu kwa mapenzi ya Mungu. 11 Kwa maana ninatamani kuwaona ninyi ili niwape zawadi ya kiroho kusudi mfanywe imara; 12 au badala yake, tutiane moyo,*+ kila mmoja kupitia imani ya mwenzake, yenu na yangu pia.
13 Lakini, akina ndugu, sitaki mkose kujua kwamba mara nyingi nilikusudia kuja kwenu ili nipate matunda kati yenu pia kama ilivyo katika mataifa mengine, lakini nimezuiwa mpaka sasa. 14 Mimi nina deni kwa Wagiriki na kwa watu wa mataifa ya kigeni,* kwa wenye hekima na wasio na akili pia: 15 kwa hiyo ninatamani kuwatangazia habari njema pia ninyi mlio huko Roma.+ 16 Kwa maana siionei aibu habari njema;+ kwa kweli, hiyo ni nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu kwa kila mtu aliye na imani,+ kwanza kwa Myahudi+ na pia kwa Mgiriki.+ 17 Kwa sababu kupitia habari njema, uadilifu wa Mungu unafunuliwa kupitia imani na kwa ajili ya imani,+ kama ilivyoandikwa: “Lakini mwadilifu ataishi kupitia imani.”+
18 Kwa kuwa ghadhabu ya Mungu+ inafunuliwa kutoka mbinguni dhidi ya watu wote wasiomwogopa Mungu na wasio waadilifu ambao wanaikandamiza kweli+ kwa njia isiyo ya uadilifu, 19 kwa sababu mambo yanayoweza kujulikana kuhusu Mungu yako wazi kabisa kati yao, kwa maana Mungu aliyaweka wazi kwao.+ 20 Kwa maana sifa zake zisizoonekana, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kupitia vitu vilivyoumbwa,+ yaani, nguvu zake za milele+ na Uungu,+ hivi kwamba hawana sababu ya kujitetea. 21 Kwa maana ingawa walimjua Mungu, hawakumtukuza yeye akiwa Mungu wala hawakumshukuru, bali walikuwa wajinga katika fikira zao na mioyo yao isiyo na ufahamu ikawa na giza.+ 22 Ingawa walidai wana hekima, wakawa wapumbavu 23 na kuugeuza utukufu wa Mungu asiyeweza kuharibika kuwa kitu kama sanamu ya mwanadamu anayeweza kuharibika* na ya ndege na viumbe wenye miguu minne na viumbe wanaotambaa.+
24 Kwa hiyo, kwa kupatana na tamaa za mioyo yao, Mungu aliwaacha katika uchafu, ili miili yao ivunjiwe heshima kati yao. 25 Waliibadili kweli ya Mungu kwa ajili ya uwongo, nao wakaabudu* uumbaji na kuutolea utumishi mtakatifu badala ya kumtolea Muumba, anayesifiwa milele. Amina. 26 Ndiyo sababu Mungu aliwaacha katika hamu isiyodhibitiwa ya ngono,+ kwa maana wanawake wao walibadili matumizi yao ya asili kuwa kinyume cha asili;+ 27 vivyo hivyo pia wanaume waliacha matumizi ya asili ya* mwanamke na kuwakiana tamaa kali za uchu wao kwa wao, wanaume kwa wanaume,+ wakitenda mambo machafu na kupokea ndani yao wenyewe adhabu* kamili, kwa sababu ya kosa lao.+
28 Kwa sababu waliona haifai kumkubali Mungu,* Mungu aliwaacha katika hali ya akili isiyokubalika, ili wafanye mambo yasiyofaa.+ 29 Nao wakajaa kila namna ya ukosefu wa uadilifu,+ uovu, pupa,*+ na ubaya, wakiwa wamejaa wivu,+ uuaji,+ mizozo, udanganyifu,+ na nia ya kuwaumiza wengine,+ wakiwa wanong’onezaji,* 30 wasengenyaji,+ wenye kumchukia Mungu, wenye dharau, wenye majivuno, wenye kujidai, wenye kutunga mambo mabaya,* wasiotii wazazi,+ 31 wasio na uelewaji,+ wanaovunja makubaliano, wasio na upendo wa asili, na wasio na rehema. 32 Ingawa wanajua vizuri amri ya uadilifu ya Mungu—kwamba wale wanaozoea kufanya mambo kama hayo wanastahili kifo+—wanaendelea kuyafanya na pia wanakubaliana na wale wanaozoea kuyafanya.
2 Kwa hiyo huwezi kujitetea, ewe mwanadamu, hata uwe nani,+ ikiwa unahukumu; kwa maana unapomhukumu mwingine, unajihukumu wewe mwenyewe, kwa sababu wewe unayehukumu umezoea kufanya mambo hayohayo.+ 2 Sasa tunajua kwamba, hukumu ya Mungu inapatana na kweli, dhidi ya wale wanaozoea kufanya mambo hayo.
3 Lakini ewe mwanadamu, unadhani utaponyoka hukumu ya Mungu unapowahukumu wale wanaozoea kufanya mambo hayo na bado wewe unayafanya? 4 Au je, wewe unadharau utajiri wa fadhili zake+ na uvumilivu*+ na subira,+ kwa sababu hujui kwamba Mungu kwa fadhili zake anajaribu kukuongoza wewe kwenye toba?+ 5 Lakini kulingana na ukaidi wako na moyo wako usiotubu, unajiwekea akiba ya ghadhabu katika siku ya ghadhabu na ya kufunuliwa kwa hukumu ya uadilifu ya Mungu.+ 6 Naye atamlipa kila mmoja kulingana na matendo yake:+ 7 uzima wa milele kwa wale wanaotafuta utukufu na heshima na kutoharibika,+ kwa uvumilivu katika kazi iliyo njema; 8 hata hivyo, kwa wale wenye ugomvi na wale wasioitii kweli lakini wanatii ukosefu wa uadilifu, kutakuwa na ghadhabu na hasira.+ 9 Kutakuwa na dhiki na taabu kwa kila mtu* anayefanya mabaya, kwanza kwa Myahudi na pia kwa Mgiriki; 10 bali utukufu na heshima na amani kwa kila mtu anayefanya mema, kwanza kwa Myahudi+ na pia kwa Mgiriki.+ 11 Kwa maana Mungu hana ubaguzi.+
12 Kwa kuwa wote waliofanya dhambi bila sheria wataangamia pia bila sheria;+ bali wote waliofanya dhambi chini ya sheria watahukumiwa kwa sheria.+ 13 Kwa maana wale wanaosikia sheria sio waadilifu mbele za Mungu, bali wale wanaoshika sheria watatangazwa kuwa waadilifu.+ 14 Kwa maana watu wa mataifa wasio na sheria+ wanapofanya kwa asili mambo ya sheria, watu hawa, ingawa hawana sheria, wao ni sheria kwao wenyewe. 15 Wao wenyewe wanaonyesha kuwa yaliyomo katika sheria yameandikwa ndani ya mioyo yao, huku dhamiri yao ikiwatolea ushahidi, na kwa* fikira zao wenyewe wanashtakiwa au hata kutetewa. 16 Hili litatendeka siku ambayo Mungu kupitia Kristo Yesu atahukumu mambo ya siri ya wanadamu,+ kulingana na habari njema ninayoitangaza.
17 Sasa, ikiwa wewe ni Myahudi kwa jina+ na unategemea sheria na kujivunia Mungu, 18 na unajua mapenzi yake na unakubali mambo yaliyo bora kabisa kwa sababu unafundishwa* kutokana na Sheria,+ 19 nawe unasadiki kwamba wewe ni kiongozi wa vipofu, nuru kwa walio gizani, 20 mrekebishaji wa wale wasio na akili, mwalimu wa watoto wadogo, na una picha ya ujuzi na ya ile kweli katika Sheria— 21 hata hivyo, je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe?+ Wewe unayehubiri, “Usiibe,”+ je, wewe huiba? 22 Wewe unayesema, “Usifanye uzinzi,”+ je, wewe hufanya uzinzi? Wewe unayechukia sanamu, je, wewe huiba katika mahekalu? 23 Wewe unayejivunia sheria, je, unamvunjia Mungu heshima kwa kuivunja Sheria? 24 Kwa maana “watu wanalikufuru jina la Mungu miongoni mwa mataifa kwa sababu yenu,” kama ilivyoandikwa.+
25 Kwa kweli, kutahiriwa+ kuna faida ikiwa tu umezoea kuifuata sheria;+ lakini ikiwa wewe huvunja sheria, kutahiriwa kwako kumekuwa kutotahiriwa. 26 Kwa hiyo, ikiwa mtu asiyetahiriwa+ huyashika matakwa ya uadilifu ya Sheria, kutotahiriwa kwake kutahesabiwa kuwa kutahiriwa, sivyo?+ 27 Na mtu asiyetahiriwa kimwili, akiishika Sheria, atakuhukumu wewe ambaye huvunja sheria ingawa una sheria zilizoandikwa na umetahiriwa. 28 Kwa kuwa yeye si Myahudi aliye hivyo kwa nje,+ wala kutahiriwa si kitu kilicho nje, juu ya mwili.+ 29 Bali yeye ni Myahudi aliye hivyo kwa ndani,+ na kutahiriwa kwake ni kule kwa moyo+ kupitia roho, wala si kupitia sheria zilizoandikwa.+ Sifa ya mtu huyo hutoka kwa Mungu, si kwa wanadamu.+
3 Basi, Myahudi ana ubora gani, au kutahiriwa kuna faida gani? 2 Ni nyingi katika kila njia. Kwanza kabisa, wao walikabidhiwa maneno matakatifu ya Mungu.+ 3 Basi, hali ikoje? Ikiwa wengine walikosa imani, je, ukosefu wao wa imani utaondoa uaminifu wa Mungu? 4 La hasha! Bali Mungu na aonekane kuwa wa kweli,+ hata ikiwa kila mwanadamu ataonekana kuwa mwongo,+ kama ilivyoandikwa: “Ili uthibitike kuwa mwadilifu katika maneno yako na ushinde wakati unapohukumiwa.”+ 5 Hata hivyo, ikiwa ukosefu wetu wa uadilifu unaonyesha wazi uadilifu wa Mungu, tuseme nini? Mungu hakosi kutenda kwa haki anapoonyesha ghadhabu yake, sivyo? (Ninaongea kama mwanadamu.) 6 Hapana! Ikiwa hivyo, Mungu atauhukumu ulimwengu jinsi gani?+
7 Lakini ikiwa kupitia uwongo wangu kweli ya Mungu imeonekana wazi zaidi kwa utukufu wake, kwa nini mimi pia ninahukumiwa kuwa mtenda dhambi? 8 Na kwa nini tusiseme, kama watu fulani wanavyodai kwa uwongo kwamba tunasema, “Tufanye mambo mabaya ili mambo mema yaje”? Hukumu dhidi ya watu hao inapatana na haki.+
9 Tuseme nini basi? Je, sisi tuna hali bora zaidi? Sivyo hata kidogo! Kwa maana hapo juu tumefanya shtaka kwamba Wayahudi na vilevile Wagiriki wote wako chini ya dhambi;+ 10 kama ilivyoandikwa: “Hakuna mwanadamu mwadilifu, hakuna hata mmoja;+ 11 hakuna yeyote aliye na ufahamu; hakuna yeyote anayemtafuta Mungu. 12 Watu wote wamegeuka kando, wote wamekuwa wasiofaa kitu; hakuna yeyote anayetenda kwa fadhili, hakuna hata mmoja.”+ 13 “Koo lao ni kaburi lililo wazi, wamedanganya kwa ndimi zao.”+ “Sumu ya nyoka iko nyuma ya midomo yao.”+ 14 “Na kinywa chao kimejaa kulaani na uchungu.”+ 15 “Miguu yao inaharakisha kwenda kumwaga damu.”+ 16 “Njia zao zina uharibifu na maumivu, 17 nao hawajaijua njia ya amani.”+ 18 “Hakuna hofu ya Mungu mbele ya macho yao.”+
19 Sasa tunajua kwamba mambo yote ambayo Sheria inasema, inawaambia wale walio chini ya Sheria, ili kila kinywa kinyamazishwe na ulimwengu wote ustahili adhabu kutoka kwa Mungu.+ 20 Kwa hiyo, hakuna mtu yeyote atakayetangazwa* kuwa mwadilifu mbele zake kupitia matendo ya sheria,+ kwa maana kupitia sheria tunapata ujuzi sahihi kuhusu dhambi.+
21 Lakini sasa uadilifu wa Mungu umefunuliwa bila sheria,+ kama inavyoshuhudiwa na Sheria na Manabii,+ 22 ndiyo, uadilifu wa Mungu kupitia imani katika Yesu Kristo, kwa wote walio na imani. Kwa maana hakuna tofauti.+ 23 Kwa maana wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu,+ 24 nayo ni zawadi ya bure+ kwamba wanatangazwa kuwa waadilifu kwa fadhili zake zisizostahiliwa+ kupitia kuachiliwa huru kwa njia ya fidia ambayo Kristo Yesu alilipa.+ 25 Mungu alimtoa kuwa dhabihu ya upatanisho*+ kupitia imani katika damu yake.+ Ilikuwa hivyo ili kuonyesha uadilifu wake mwenyewe, kwa sababu Mungu kwa uvumilivu* wake alikuwa akizisamehe dhambi zilizofanywa wakati uliopita. 26 Ilikuwa hivyo ili kuonyesha uadilifu wake+ katika majira haya, ili awe mwadilifu hata anapomtangaza kuwa mwadilifu mtu aliye na imani katika Yesu.+
27 Basi, je, tuna sababu ya kujisifu? Hatuna sababu. Kupitia sheria gani? Ile ya matendo?+ Hapana, bali kupitia sheria ya imani. 28 Kwa maana tunajua kwamba mtu hutangazwa kuwa mwadilifu kwa imani bila matendo ya sheria.+ 29 Au je, yeye ni Mungu wa Wayahudi peke yao?+ Je, yeye si Mungu wa watu wa mataifa pia?+ Ndiyo, pia wa watu wa mataifa.+ 30 Kwa kuwa Mungu ni mmoja,+ atawatangaza watu waliotahiriwa kuwa waadilifu+ kutokana na imani na watu wasiotahiriwa kuwa waadilifu+ kupitia imani yao. 31 Basi, je, tunaifuta sheria kupitia imani yetu? La hasha! Badala yake, tunaiunga mkono sheria.+
4 Ikiwa ni hivyo, tutasema alipata faida gani Abrahamu, babu yetu kulingana na mwili? 2 Kwa mfano, ikiwa Abrahamu alitangazwa kuwa mwadilifu kwa sababu ya matendo, angekuwa na sababu ya kujisifu, lakini si mbele za Mungu. 3 Kwani andiko linasema nini? “Abrahamu alikuwa na imani katika Yehova,* na hilo likahesabiwa kwake kuwa uadilifu.”+ 4 Basi kwa mtu anayefanya kazi, malipo yake hayahesabiwi kuwa fadhili zisizostahiliwa bali ni deni. 5 Kwa upande mwingine, mtu asiyefanya kazi bali anaweka imani katika Yule anayemtangaza kuwa mwadilifu mtu asiyemwogopa Mungu, imani yake inahesabiwa kuwa ni uadilifu.+ 6 Kama vile Daudi pia anavyosema kuhusu furaha ya mtu ambaye Mungu humhesabu kuwa mwadilifu bila matendo: 7 “Wenye furaha ni wale ambao matendo yao ya kuasi sheria yamesamehewa na ambao dhambi zao zimefunikwa;* 8 mwenye furaha ni mtu ambaye Yehova* hatahesabu dhambi yake kamwe.”+
9 Basi, je, furaha hiyo huja tu kwa watu waliotahiriwa au pia kwa watu wasiotahiriwa?+ Kwa maana tunasema: “Imani ya Abrahamu ilihesabiwa kwake kuwa uadilifu.”+ 10 Basi, ilihesabiwa kuwa uadilifu chini ya hali gani? Alipokuwa ametahiriwa au kabla ya kutahiriwa? Ni kabla ya kutahiriwa. 11 Naye alipokea ishara+—yaani, kutahiriwa—kuwa muhuri wa* uadilifu kwa imani aliyokuwa nayo alipokuwa katika hali yake ya kutotahiriwa, ili awe baba ya wale wote walio na imani+ ingawa hawajatahiriwa, kusudi wahesabiwe kuwa waadilifu; 12 na ili awe baba ya uzao uliotahiriwa, si kwa wale tu wanaoshikamana na kutahiriwa, bali pia kwa wale wanaotembea kwa utaratibu katika hatua za imani ambayo baba yetu Abrahamu+ alikuwa nayo katika hali ya kutotahiriwa.
13 Kwa maana Abrahamu au uzao wake* hawakupata ahadi kwamba atakuwa mrithi wa ulimwengu kupitia sheria,+ bali kupitia uadilifu kwa imani.+ 14 Kwa maana ikiwa wale wanaoshika sheria ni warithi, imani inakuwa isiyofaa kitu na ahadi imefutwa. 15 Kwa kweli Sheria hutokeza ghadhabu,+ lakini pasipo na sheria, hakuna kosa lolote.+
16 Ndiyo sababu ni kupitia imani, ili iwe kulingana na fadhili zisizostahiliwa,+ kusudi ahadi iwe hakika kwa uzao wake* wote,+ si kwa wale tu wanaoshika Sheria, bali pia kwa wale wanaoshika imani ya Abrahamu, ambaye ni baba yetu sote.+ 17 (Kama tu ilivyoandikwa: “Nimekuweka uwe baba ya mataifa mengi.”)+ Hili lilikuwa machoni pa Mungu, ambaye Abrahamu alimwamini, anayewafanya wafu kuwa hai na kuyaita mambo yasiyokuwako kana kwamba yako.* 18 Ingawa hakukuwa na tumaini, lakini kwa kutegemea tumaini, alikuwa na imani kwamba angekuwa baba ya mataifa mengi kulingana na yale yaliyokuwa yamesemwa: “Ndivyo utakavyokuwa uzao wako.”*+ 19 Na ingawa imani yake haikudhoofika, alifikiria mwili wake mwenyewe, sasa ukiwa kama tayari umekufa (kwa kuwa alikuwa na umri wa karibu miaka 100),+ na pia hali ya kufa* ya tumbo la uzazi la Sara.+ 20 Lakini kwa sababu ya ahadi ya Mungu, yeye hakusitasita kwa kukosa imani; bali alikuwa mwenye nguvu kwa imani yake, akimpa Mungu utukufu 21 na akiwa na uhakika kamili kwamba Mungu alikuwa na uwezo wa kutimiza kile alichoahidi.+ 22 Kwa hiyo “ikahesabiwa kwake kuwa uadilifu.”+
23 Hata hivyo, maneno “ilihesabiwa kwake” hayakuandikwa kwa ajili yake tu,+ 24 bali pia kwa ajili yetu ambao itahesabiwa, kwa sababu tunamwamini Yeye aliyemfufua Yesu Bwana wetu kutoka kwa wafu.+ 25 Alitolewa kwa ajili ya makosa yetu+ na kufufuliwa kwa ajili ya kututangaza sisi kuwa waadilifu.+
5 Basi, kwa kuwa sasa tumetangazwa kuwa waadilifu kutokana na imani,+ na tufurahie amani* pamoja na Mungu kupitia Bwana wetu Yesu Kristo,+ 2 ambaye kupitia kwake sisi pia tumepata fursa ya kuingia kwa imani katika fadhili hizi zisizostahiliwa ambamo sasa tunasimama;+ na tushangilie,* kwa kutegemea tumaini la utukufu wa Mungu. 3 Si hilo tu, bali na tushangilie* tukiwa katika dhiki,+ kwa kuwa tunajua kwamba dhiki hutokeza uvumilivu;+ 4 nao uvumilivu, hali yenye kukubaliwa;+ nayo hali yenye kukubaliwa, tumaini,+ 5 nalo tumaini halikatishi tamaa;+ kwa sababu upendo wa Mungu umemiminwa ndani ya mioyo yetu kupitia roho takatifu, ambayo tulipewa.+
6 Kwa maana, kwa kweli, tulipokuwa bado dhaifu,+ Kristo alikufa wakati uliowekwa kwa ajili ya watu wasiomwogopa Mungu. 7 Kwa maana ni vigumu kwa yeyote kufa kwa ajili ya mtu mwadilifu; hata hivyo labda mtu anaweza kuthubutu kufa kwa ajili ya mtu mwema. 8 Lakini Mungu hupendekeza upendo wake kwetu kwa kuwa tulipokuwa bado watenda dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.+ 9 Kwa kuwa sasa tumetangazwa kuwa waadilifu kwa damu yake,+ tutaokolewa hata zaidi kutokana na ghadhabu kupitia yeye.+ 10 Kwa maana, ikiwa tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kupitia kifo cha Mwana wake,+ tutaokolewa hata zaidi kwa uhai wake, kwa kuwa sasa tumepatanishwa. 11 Si hilo tu, bali pia tunashangilia katika Mungu kupitia Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kupitia kwake sasa tumepokea upatanisho.+
12 Hiyo ndiyo sababu, kama vile kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi,+ basi kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi+—. 13 Kwa maana dhambi ilikuwa katika ulimwengu kabla ya Sheria, lakini mtu yeyote hahesabiwi kuwa na dhambi ikiwa hakuna sheria.+ 14 Hata hivyo, kifo kilitawala kama mfalme tangu Adamu mpaka Musa, hata juu ya wale ambao hawakuwa wamefanya dhambi kama vile Adamu alivyofanya kosa, ambaye ni mfano wa yule aliyepaswa kuja.+
15 Lakini zawadi si kama lile kosa. Kwa maana ikiwa kwa kosa la mtu mmoja wengi walikufa, fadhili zisizostahiliwa za Mungu na zawadi yake ya bure kupitia fadhili zisizostahiliwa za mtu mmoja,+ Yesu Kristo, zilizidi* hata zaidi kwa wengi!+ 16 Pia, ile zawadi ya bure si sawa na jinsi mambo yalivyotendeka kupitia mtu mmoja aliyefanya dhambi.+ Kwa maana hukumu baada ya kosa moja ilikuwa hatia,+ lakini zawadi baada ya makosa mengi ilikuwa tangazo la uadilifu.+ 17 Kwa maana ikiwa kwa kosa la mtu mmoja kifo kilitawala kama mfalme kupitia mtu huyo,+ wale wanaopokea wingi wa fadhili zisizostahiliwa na zawadi ya bure ya uadilifu+ watatawala hata zaidi wakiwa wafalme+ katika uzima kupitia mtu mmoja, Yesu Kristo!+
18 Kwa hiyo basi, kama vile kupitia kosa moja matokeo kwa watu wa namna zote yalikuwa kuhukumiwa hatia,+ vivyo hivyo kupitia tendo moja la kutetewa matokeo kwa watu wa namna zote+ ni wao kutangazwa kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima.+ 19 Kwa maana kama vile kupitia kutotii kwa mtu mmoja wengi walifanywa kuwa watenda dhambi,+ vivyo hivyo pia kupitia kutii kwa mtu mmoja wengi watafanywa kuwa waadilifu.+ 20 Basi Sheria ilikuja ili makosa yaongezeke.+ Lakini mahali ambapo dhambi ilizidi, fadhili zisizostahiliwa zilizidi hata zaidi. 21 Kwa kusudi gani? Ili kama vile dhambi ilivyotawala kama mfalme pamoja na kifo,+ vivyo hivyo pia fadhili zisizostahiliwa zitawale kama mfalme kupitia uadilifu na kuleta uzima wa milele kupitia Yesu Kristo Bwana wetu.+
6 Basi tuseme nini? Je, tuendelee kuwa katika dhambi, ili fadhili zisizostahiliwa ziongezeke? 2 La hasha! Kwa kuwa tulikufa kuhusiana na dhambi,+ tunawezaje kuendelea kuishi tena katika dhambi?+ 3 Au je, hamjui kwamba sisi sote tuliobatizwa katika Kristo Yesu+ tulibatizwa katika kifo chake?+ 4 Basi tulizikwa pamoja naye kupitia ubatizo wetu katika kifo chake,+ ili kama vile Kristo alivyofufuliwa kutoka kwa wafu kupitia utukufu wa Baba, vivyo hivyo sisi pia tunapaswa tutembee katika hali mpya ya uzima.+ 5 Ikiwa tumeungana pamoja naye katika mfano wa kifo chake,+ hakika sisi pia tutaunganishwa pamoja naye katika mfano wa ufufuo wake.+ 6 Kwa maana tunajua kwamba utu wetu wa zamani ulitundikwa mtini pamoja naye,+ ili mwili wetu wenye dhambi usiwe na nguvu,+ ili tusiendelee kuwa watumwa wa dhambi.+ 7 Kwa maana yule ambaye amekufa ameondolewa* hatia ya dhambi yake.
8 Isitoshe, ikiwa tumekufa pamoja na Kristo, tunaamini kwamba tutaishi pia pamoja naye. 9 Kwa maana tunajua kwamba Kristo, kwa kuwa sasa amefufuliwa kutoka kwa wafu,+ hatakufa tena;+ kifo si bwana juu yake tena. 10 Kwa maana kifo alichokufa, alikufa kuhusiana na dhambi* mara moja kwa wakati wote,+ lakini uhai anaoishi, anaishi kuhusiana na Mungu. 11 Vivyo hivyo ninyi, mjihesabu kuwa wafu kuhusiana na dhambi lakini walio hai kuhusiana na Mungu kupitia Kristo Yesu.+
12 Kwa hiyo, msiruhusu dhambi iendelee kutawala kama mfalme katika miili yenu inayoweza kufa+ hivi kwamba mzitii tamaa zake. 13 Wala msiendelee kuitoa miili yenu* kwa dhambi kuwa silaha za ukosefu wa uadilifu, bali jitoeni wenyewe kwa Mungu kama walio hai kutoka kwa wafu, pia toeni miili yenu* kwa Mungu kuwa silaha za uadilifu.+ 14 Kwa maana dhambi haipaswi kuwa bwana juu yenu, kwa kuwa ninyi hamko chini ya sheria+ bali chini ya fadhili zisizostahiliwa.+
15 Tuseme nini basi? Je, tufanye dhambi kwa sababu hatuko chini ya sheria bali chini ya fadhili zisizostahiliwa?+ La hasha! 16 Je, hamjui kwamba mkijitoa kwa yeyote kuwa watumwa watiifu, ninyi ni watumwa wa yule mnayemtii,+ ama watumwa wa dhambi+ inayotokeza kifo+ au wa utii unaotokeza uadilifu? 17 Lakini shukrani kwa Mungu kwamba ingawa wakati fulani mlikuwa watumwa wa dhambi, sasa mmekuwa watiifu kutoka moyoni kwa kielelezo cha fundisho mlilokabidhiwa. 18 Ndiyo, kwa kuwa mliwekwa huru kutoka katika dhambi,+ mmekuwa watumwa wa uadilifu.+ 19 Ninazungumza kwa maneno ya kibinadamu kwa sababu ya udhaifu wa miili yenu; kwa maana kama mlivyovitoa viungo vyenu kuwa watumwa wa mambo machafu na uasi sheria unaotokeza uasi sheria, basi sasa vitoeni viungo vyenu viwe watumwa wa uadilifu unaotokeza utakatifu.+ 20 Kwa maana mlipokuwa watumwa wa dhambi, mlikuwa huru kuhusiana na uadilifu.
21 Basi, mlikuwa mkizaa matunda gani wakati huo? Mambo ambayo sasa mnayaonea aibu. Kwa maana mwisho wa mambo hayo ni kifo.+ 22 Hata hivyo, sasa, kwa vile mliwekwa huru kutoka katika dhambi na kuwa watumwa wa Mungu, mnazaa matunda katika utakatifu,+ na mwisho ni uzima wa milele.+ 23 Kwa maana mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo,+ lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele+ kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.+
7 Akina ndugu, je, inawezekana kwamba hamjui (kwa maana ninasema na wale wanaoijua sheria) kuwa Sheria ni bwana juu ya mtu anapokuwa hai? 2 Kwa mfano, mwanamke aliyeolewa amefungwa na sheria kwa mume wake akiwa hai; lakini mume wake akifa, yuko huru kutoka katika sheria ya mume wake.+ 3 Hivyo basi, mume wake akiwa hai, mwanamke huyo ataitwa mzinzi ikiwa atakuwa wa mwanamume mwingine.+ Lakini mume wake akifa, yuko huru kutoka kwa sheria ya mume, basi mwanamke huyo si mzinzi ikiwa ataolewa na mwanamume mwingine.+
4 Basi, ndugu zangu, ninyi pia mlifanywa wafu kuhusiana na Sheria kupitia mwili wa Kristo, ili muwe wa mwingine,+ yule aliyefufuliwa kutoka kwa wafu,+ ili tumzalie Mungu matunda.+ 5 Kwa maana tulipokuwa tukiishi kulingana na mwili, tamaa zenye dhambi zilizoamshwa na Sheria zilikuwa zikifanya kazi katika miili yetu* ili kuzaa matunda ya kifo.+ 6 Lakini sasa tumewekwa huru kutoka katika Sheria,+ kwa sababu tumekufa kwa kile ambacho kilituzuia, ili tuwe watumwa katika maana mpya kwa roho,+ wala si katika maana ya zamani kwa sheria zilizoandikwa.+
7 Basi, tuseme nini? Je, Sheria ni dhambi? La hasha! Kwa kweli, singejua dhambi ikiwa Sheria haingekuwapo.+ Kwa mfano, mimi singejua tamaa ikiwa Sheria haingesema: “Usitamani.”+ 8 Lakini dhambi, kwa kutumia amri hiyo ilipata nafasi ya kutokeza ndani yangu tamaa ya kila aina, kwa maana bila sheria dhambi ilikuwa imekufa.+ 9 Kwa kweli, wakati mmoja nilikuwa hai bila sheria. Lakini amri ilipofika, dhambi ikawa hai tena, lakini mimi nikafa.+ 10 Na amri iliyokuwa ya kuongoza kwenye uzima,+ niliiona kuwa inaongoza kwenye kifo. 11 Kwa maana dhambi kwa kutumia amri hiyo ilipata nafasi ya kunishawishi na kuniua kupitia amri. 12 Basi Sheria yenyewe ni takatifu, na amri ni takatifu na yenye uadilifu na ni njema.+
13 Kwa hiyo, je, lililo jema lilinisababishia kifo? La hasha! Lakini dhambi ilifanya hivyo, ili ionyeshwe kuwa dhambi ndiyo inayoniletea kifo kupitia lile lililo jema,+ ili kupitia amri dhambi iwe mbaya zaidi.+ 14 Kwa maana tunajua kwamba Sheria ni ya kiroho, lakini mimi ni wa kimwili, nimeuzwa kwenye dhambi.+ 15 Kwa kuwa sielewi kile ninachokifanya. Kwa maana sifanyi kile ninachotaka, bali ninafanya kile ninachochukia. 16 Hata hivyo, ikiwa ninafanya jambo nisilotaka, nakubali kwamba Sheria ni nzuri. 17 Lakini sasa si mimi tena ninayelifanya, bali ni dhambi inayokaa ndani yangu.+ 18 Kwa maana najua kwamba ndani yangu, yaani, katika mwili wangu, halikai jambo lolote jema; kwa kuwa nina tamaa ya kufanya mambo mema lakini sina uwezo wa kuyafanya.+ 19 Kwa maana sifanyi jambo jema ninalotaka, bali ninafanya jambo baya nisilotaka. 20 Basi, ikiwa ninafanya jambo nisilotaka, si mimi tena ninayelifanya, bali ni dhambi inayokaa ndani yangu.
21 Basi, mimi naona sheria hii katika hali yangu: Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.+ 22 Kwa kweli naipenda sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani,+ 23 lakini ninaona ndani ya mwili wangu* sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu+ na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi+ iliyo ndani ya mwili wangu.* 24 Maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki? 25 Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu! Basi, kwa akili yangu mimi ni mtumwa wa sheria ya Mungu, lakini kwa mwili wangu mimi ni mtumwa wa sheria ya dhambi.+
8 Kwa hiyo, wale walio katika muungano na Kristo Yesu hawana hukumu ya hatia. 2 Kwa maana sheria ya roho ambayo hutokeza uzima katika muungano na Kristo Yesu imewaweka ninyi huru+ kutoka katika sheria ya dhambi na kifo. 3 Kile ambacho Sheria ilishindwa kufanya+ kwa sababu ilikuwa dhaifu+ kupitia mwili, Mungu alifanya kwa kumtuma Mwana wake mwenyewe+ akiwa katika mfano wa mwili wenye dhambi+ na kuhusu dhambi, akiihukumu dhambi katika mwili, 4 ili takwa la uadilifu la Sheria litimizwe ndani yetu+ sisi tunaotembea, si kulingana na mwili, bali kulingana na roho.+ 5 Kwa kuwa wale wanaoishi kulingana na mwili hukaza akili zao kwenye mambo ya mwili,+ lakini wale wanaoishi kulingana na roho kwenye mambo ya roho.+ 6 Kwa maana kukaza akili kwenye mwili humaanisha kifo,+ lakini kukaza akili kwenye roho humaanisha uzima na amani;+ 7 kwa sababu kukaza akili kwenye mwili humaanisha uadui na Mungu, kwa kuwa mwili haujitiishi kwa sheria ya Mungu,+ nao kwa kweli hauwezi kujitiisha. 8 Basi wale wanaopatana na mwili hawawezi kumpendeza Mungu.
9 Hata hivyo, ninyi hampatani na mwili, bali mnapatana na roho,+ ikiwa kweli roho ya Mungu inakaa ndani yenu. Lakini ikiwa mtu yeyote hana roho ya Kristo, mtu huyo si wake. 10 Lakini ikiwa Kristo yuko katika muungano pamoja nanyi,+ mwili umekufa kwa sababu ya dhambi, bali roho ni uzima kwa sababu ya uadilifu. 11 Basi, ikiwa roho ya yule aliyemfufua Yesu kutoka kwa wafu inakaa ndani yenu, yule aliyemfufua Kristo Yesu kutoka kwa wafu+ ataifanya pia miili yenu inayoweza kufa iwe hai+ kupitia roho yake inayokaa ndani yenu.
12 Basi, akina ndugu, sisi tuna wajibu, si kwa mwili ili tuishi kulingana na mwili;+ 13 kwa maana ikiwa mnaishi kulingana na mwili hakika ninyi mtakufa; bali mkiyaua mazoea ya mwili+ kwa roho, mtaishi.+ 14 Kwa maana wote wanaoongozwa na roho ya Mungu, kwa kweli ndio wana wa Mungu.+ 15 Kwa maana hamkupokea roho ya utumwa inayosababisha woga tena, bali mlipokea roho ya kufanywa kuwa wana, roho ambayo kupitia hiyo tunapaza sauti: “Abba,* Baba!”+ 16 Roho yenyewe hutoa ushahidi pamoja na roho yetu+ kwamba sisi ni watoto wa Mungu.+ 17 Basi, ikiwa sisi ni watoto, sisi pia ni warithi—warithi wa Mungu kwelikweli, lakini warithi pamoja+ na Kristo—mradi tu tunateseka pamoja+ ili pia tutukuzwe pamoja.+
18 Kwa maana ninaona kwamba mateso ya wakati huu si kitu yakilinganishwa na utukufu utakaofunuliwa ndani yetu.+ 19 Kwa kuwa uumbaji unangojea na kutazamia kwa hamu kufunuliwa kwa wana wa Mungu.+ 20 Kwa maana uumbaji ulitiishwa chini ya ubatili,+ si kwa mapenzi yake wenyewe bali kupitia yule aliyeutiisha, kwa msingi wa tumaini 21 kwamba uumbaji wenyewe pia utawekwa huru+ kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu. 22 Kwa maana tunajua kwamba uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja mpaka sasa. 23 Si hilo tu, bali sisi wenyewe pia tulio na matunda ya kwanza, yaani, ile roho, ndiyo, sisi wenyewe tunaugua ndani yetu wenyewe,+ huku tukingojea kwa hamu kufanywa kuwa wana,+ kuachiliwa huru kutoka kwenye miili yetu kupitia fidia. 24 Kwa maana tuliokolewa katika tumaini hili; lakini tumaini linaloonekana si tumaini, kwa kuwa mtu anapoona kitu, je, yeye hukitumainia? 25 Lakini tukitumainia+ kile ambacho hatuoni,+ sisi huendelea kukisubiri kwa hamu na uvumilivu.+
26 Vivyo hivyo, roho pia hutoa msaada kwa ajili ya udhaifu wetu;+ kwa maana tatizo ni kwamba hatujui kile tunachopaswa kusali kuhusu kama tunavyohitaji, lakini roho yenyewe hutuombea kwa kuugua kusikotamkwa.* 27 Lakini yule anayechunguza mioyo+ anajua maana ya roho, kwa sababu inaomba kupatana na Mungu kwa ajili ya watakatifu.
28 Tunajua kwamba Mungu huzifanya kazi zake zote zishirikiane pamoja kwa ajili ya mema ya wale wanaompenda Mungu, wale ambao wameitwa kulingana na kusudi lake;+ 29 kwa sababu wale aliowatambua kwanza, aliwachagua awali pia wafananishwe na mfano wa Mwana wake,+ ili awe mzaliwa wa kwanza+ kati ya ndugu wengi.+ 30 Isitoshe, wale aliowachagua awali+ ndio aliowaita pia;+ na wale aliowaita ndio aliowatangaza kuwa waadilifu pia.+ Mwishowe wale aliowatangaza kuwa waadilifu ndio aliowatukuza pia.+
31 Basi, tuseme nini kuhusu mambo haya? Ikiwa Mungu yuko upande wetu, ni nani atakayekuwa dhidi yetu?+ 32 Kwa kuwa hakusita kumtoa hata Mwana wake mwenyewe bali alimkabidhi kwa ajili yetu sote,+ je, hatatupatia pia pamoja naye kwa fadhili vitu vingine vyote? 33 Ni nani atakayewashtaki waliochaguliwa wa Mungu?+ Mungu Ndiye anayewatangaza kuwa waadilifu.+ 34 Ni nani atakayewahukumu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa, ndiyo, isitoshe yeye ndiye aliyefufuliwa, aliye kwenye mkono wa kuume wa Mungu+ na ambaye pia hutuombea.+
35 Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo?+ Je, ni dhiki au taabu au mateso au njaa au uchi au hatari au upanga?+ 36 Kama ilivyoandikwa: “Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa; tumehesabiwa kuwa kondoo wa kuchinjwa.”+ 37 Badala yake, katika mambo haya yote tunatoka tukiwa tumeshinda kabisa+ kupitia yule aliyetupenda. 38 Kwa maana nimesadiki kwamba wala kifo wala uzima wala malaika wala serikali wala mambo yaliyopo sasa wala mambo yatakayokuja wala nguvu+ 39 wala kimo wala kina wala uumbaji mwingine wowote havitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.
9 Ninasema kweli katika Kristo; sisemi uwongo, kama dhamiri yangu inavyonitolea ushahidi katika roho takatifu, 2 kwamba nina huzuni kubwa na maumivu yasiyoisha moyoni mwangu. 3 Kwa maana ningetamani mimi mwenyewe nitenganishwe na Kristo, niwe aliyelaaniwa kwa ajili ya ndugu zangu, watu wangu wa ukoo kulingana na mwili, 4 ambao ni Waisraeli. Wao ndio waliofanywa kuwa wana+ na kupewa utukufu na maagano+ na Sheria+ na utumishi mtakatifu+ na ahadi.+ 5 Wao ni uzao wa mababu,+ na Kristo alitoka kwao kulingana na mwili.+ Mungu, aliye juu ya wote, asifiwe milele. Amina.
6 Hata hivyo, si kwamba neno la Mungu limeshindwa. Kwa maana si wote wanaotokana na Israeli ni “Israeli” kihalisi.+ 7 Wala si wote walio watoto kwa sababu wao ni uzao wa* Abrahamu;+ badala yake, “Ule utakaoitwa uzao wako* utapitia kwa Isaka.”+ 8 Yaani, watoto katika mwili si watoto wa Mungu kihalisi,+ lakini watoto kupitia ahadi+ ndio wanaohesabiwa kuwa uzao.* 9 Kwa maana neno la ahadi lilisema hivi: “Nitakuja wakati huuhuu, na Sara atakuwa na mwana.”+ 10 Lakini si wakati huo tu, bali pia Rebeka alipopata mimba ya mapacha kupitia yule mwanamume mmoja, Isaka babu yetu;+ 11 kwa maana walipokuwa bado hawajazaliwa wala kufanya jambo lolote jema au baya, ili kusudi la Mungu kuhusu kuchagua liendelee kutegemea, si matendo, bali Yule ambaye huita, 12 Rebeka aliambiwa: “Mkubwa atakuwa mtumwa wa mdogo.”+ 13 Kama ilivyoandikwa: “Nilimpenda Yakobo, lakini nikamchukia Esau.”+
14 Basi, tuseme nini? Je, Mungu ana ukosefu wa haki? La hasha!+ 15 Kwa maana anamwambia Musa: “Nitamwonyesha rehema yeyote ninayetaka kumwonyesha rehema, nami nitamhurumia yeyote ninayetaka kumhurumia.”+ 16 Hivyo basi, haitegemei jinsi mtu anavyotamani au jitihada zake,* bali inategemea Mungu, aliye na rehema.+ 17 Kwa maana andiko linamwambia Farao: “Kwa sababu hii nimekuacha ubaki: ili nionyeshe nguvu zangu kuhusiana na wewe na ili jina langu litangazwe katika dunia yote.”+ 18 Hivyo basi, yeye humwonyesha rehema yeyote anayetaka, lakini yeye humwacha yeyote anayetaka awe mkaidi.+
19 Kwa hiyo utaniuliza: “Kwa nini bado analaumu? Kwa maana ni nani ambaye amepinga mapenzi yake?” 20 Lakini ewe mwanadamu wewe ni nani hata uthubutu kumjibu Mungu?+ Je, kitu kilichofinyangwa kitamwambia yule aliyekifinyanga: “Kwa nini ulinitengeneza hivi?”+ 21 Kwani, je, mfinyanzi hana mamlaka juu ya udongo+ kufanya kutokana na donge lilelile chombo kimoja kwa matumizi yenye kuheshimika, na kingine kwa matumizi yasiyo ya kuheshimika? 22 Inakuwaje basi, ikiwa Mungu, ingawa alikuwa na nia ya kuonyesha ghadhabu yake na kujulisha nguvu zake, alivumilia kwa subira nyingi vyombo vya ghadhabu vilivyo tayari kwa ajili ya uharibifu? 23 Na ikiwa hilo lilifanywa ili ajulishe utajiri wa utukufu wake kwa vyombo vya rehema,+ alivyotayarisha awali kwa ajili ya utukufu, 24 yaani, sisi, ambao alituita si kutoka kati ya Wayahudi peke yao bali pia kutoka kati ya mataifa,+ kuna ubaya gani? 25 Ni kama anavyosema pia katika Hosea: “Wale ambao si watu wangu+ nitawaita ‘watu wangu,’ na mwanamke ambaye hakupendwa, nitamwita ‘mpendwa’;+ 26 na mahali ambapo waliambiwa, ‘Ninyi si watu wangu,’ hapo wataitwa ‘wana wa Mungu aliye hai.’”+
27 Isitoshe, Isaya anapaza sauti kuhusu Israeli: “Ijapokuwa idadi ya wana wa Israeli huenda ikawa kama chembe za mchanga wa bahari, ni watu wachache tu waliobaki watakaookolewa.+ 28 Kwa maana Yehova* atatoza hesabu duniani, na kuimaliza na kuifupisha.”*+ 29 Pia, kama Isaya alivyotabiri: “Kama Yehova* wa majeshi hangetuachia uzao,* tungekuwa kama Sodoma, na tungefanana na Gomora.”+
30 Basi, tuseme nini? Kwamba watu wa mataifa, ingawa hawakuwa wakiufuatilia uadilifu,+ waliufikia uadilifu, uadilifu unaotokana na imani;+ 31 lakini Israeli, ingawa walikuwa wakiifuatilia sheria ya uadilifu, hawakuifikia sheria. 32 Kwa sababu gani? Kwa sababu waliifuatilia, si kwa imani, bali kama kwa matendo. Walijikwaa kwenye “jiwe la kukwaza”;+ 33 kama ilivyoandikwa: “Tazama! Ninaweka katika Sayuni jiwe+ la kukwaza na mwamba wa kuangusha, lakini yeye anayemwamini hatakata tamaa.”+
10 Akina ndugu, nia njema ya moyo wangu na dua yangu kwa Mungu kwa ajili yao, kwa kweli, ni kwa ajili ya wokovu wao.+ 2 Kwa maana ninawatolea ushahidi kwamba wana bidii kwa ajili ya Mungu,+ lakini si kulingana na ujuzi sahihi. 3 Kwa sababu ya kutojua uadilifu wa Mungu+ bali wakijaribu kujiwekea uadilifu wao wenyewe,+ hawakujitiisha kwa uadilifu wa Mungu.+ 4 Kwa maana Kristo ndiye mwisho wa Sheria,+ ili kila mtu aliye na imani* awe na uadilifu.+
5 Kwa kuwa Musa anaandika hivi kuhusu uadilifu kupitia Sheria: “Mtu anayefanya mambo hayo ataishi kupitia mambo hayo.”+ 6 Lakini uadilifu unaotokana na imani husema: “Usiseme moyoni mwako,+ ‘Ni nani atakayepanda juu mbinguni?’+ yaani, kumleta Kristo chini, 7 au, ‘Ni nani atakayeshuka katika shimo?’*+ yaani, kumleta Kristo juu kutoka kwa wafu.” 8 Lakini linasema nini? “Neno hilo liko karibu nawe, katika kinywa chako na katika moyo wako mwenyewe”;+ yaani, “neno” la imani, ambalo sisi tunahubiri. 9 Kwa maana ukitangaza waziwazi kwa kinywa chako kwamba Yesu ni Bwana,+ na kuwa na imani moyoni mwako kwamba Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, utaokolewa. 10 Kwa sababu kwa moyo mtu huwa na imani ili apate uadilifu, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la hadharani+ ili apate wokovu.
11 Kwa kuwa andiko linasema: “Yeyote anayemwamini hatakata tamaa.”+ 12 Kwa maana hakuna tofauti kati ya Myahudi na Mgiriki.+ Kuna Bwana yuleyule juu ya wote, aliye tajiri* kwa wote wanaomwitia. 13 Kwa maana “kila mtu anayeliitia jina la Yehova* ataokolewa.”+ 14 Hata hivyo, watawezaje kumwitia ikiwa hawajamwamini? Nao watamwaminije yule ambaye hawajamsikia? Nao watasikiaje bila mtu wa kuhubiri? 15 Nao watahubirije isipokuwa wawe wametumwa?+ Kama ilivyoandikwa: “Jinsi inavyopendeza miguu ya wale wanaotangaza habari njema ya mambo mema!”+
16 Hata hivyo, si wote waliotii habari njema. Kwa maana Isaya anasema: “Yehova,* ni nani ambaye ameamini jambo alilosikia kutoka kwetu?”*+ 17 Kwa hiyo imani hufuata jambo lililosikiwa.+ Nalo jambo lililosikiwa ni kupitia neno kumhusu Kristo. 18 Lakini ninauliza, je, walikosa kusikia? Kwa kweli, “sauti yao ilifika katika dunia yote, na ujumbe wao ulifika mpaka kwenye miisho ya dunia inayokaliwa.”+ 19 Lakini ninauliza, je, kweli Israeli walikosa kujua?+ Kwanza Musa anasema: “Nitawachochea muwe na wivu kupitia lile ambalo si taifa; nitawachochea muwe na hasira kali kupitia taifa lenye ujinga.”+ 20 Lakini Isaya anakuwa na ujasiri sana na kusema: “Wale ambao hawakuwa wakinitafuta walinipata;+ wale ambao hawakuwa wakiuliza juu yangu walinijua.”+ 21 Lakini anasema kuhusiana na Israeli: “Mchana kutwa nimewanyooshea mikono yangu watu wasiotii na wakaidi.”+
11 Basi ninauliza, je, Mungu aliwakataa watu wake?+ La hasha! Kwa maana mimi pia ni Mwisraeli, wa uzao wa* Abrahamu, kutoka kabila la Benjamini. 2 Mungu hakuwakataa watu wake, aliowatambua kwanza.+ Je, hamjui andiko linavyosema kumhusu Eliya, anapomsihi Mungu dhidi ya Israeli? 3 “Yehova,* wamewaua manabii wako, wamezibomoa madhabahu zako, nami peke yangu nimebaki, na sasa wanajaribu kuniua.”*+ 4 Lakini neno la Mungu linamwambia nini? “Nimeacha watu 7,000 kwa ajili yangu, watu ambao hawakumpigia goti Baali.”+ 5 Basi, kwa njia hiyohiyo, wakati huu pia, kuna mabaki kulingana na kuchaguliwa+ kupitia fadhili zisizostahiliwa. 6 Basi ikiwa ni kupitia fadhili zisizostahiliwa,+ si kupitia matendo tena;+ la sivyo, fadhili zisizostahiliwa hazingekuwa tena fadhili zisizostahiliwa.
7 Tuseme nini, basi? Jambo lilelile ambalo Israeli anatafuta kwa bidii hakulipata, lakini wale waliochaguliwa walilipata.+ Hisia za wale wengine zilifanywa kuwa nzito,+ 8 kama ilivyoandikwa: “Mungu amewapa roho ya usingizi mzito,+ macho yasiyoona na masikio yasiyosikia, mpaka leo hii.”+ 9 Pia, Daudi anasema: “Meza yao na iwe kitu kinachonasa na mtego na kikwazo na malipo kwao. 10 Acha macho yao yatiwe giza wasiweze kuona, na sikuzote uwafanye wainamishe migongo yao.”+
11 Basi ninauliza, Je, walijikwaa na kuanguka kabisa? La hasha! Lakini kwa kujikwaa kwao, kuna wokovu kwa watu wa mataifa, ili kuwachochea wawe na wivu.+ 12 Sasa ikiwa kujikwaa kwao humaanisha utajiri kwa ulimwengu, na kupungua kwao humaanisha utajiri kwa watu wa mataifa,+ je, idadi yao kamili haitamaanisha hivyo hata zaidi?
13 Sasa ninazungumza nanyi mlio watu wa mataifa. Kwa kuwa mimi ni mtume kwa mataifa,+ ninaitukuza* huduma yangu,+ 14 ili kuona ikiwa ninaweza kwa njia fulani kuwachochea watu wangu wawe* na wivu na kuwaokoa baadhi yao. 15 Kwa maana ikiwa kutupwa kwao+ humaanisha upatanisho kwa ulimwengu, kukubaliwa kwao kutamaanisha nini isipokuwa uzima kutoka kwa wafu? 16 Isitoshe, ikiwa sehemu ya donge inayochukuliwa iwe matunda ya kwanza ni takatifu, donge lote pia ni takatifu; na ikiwa mzizi ni mtakatifu, matawi pia yako hivyo.
17 Hata hivyo, ikiwa baadhi ya matawi yalikatwa, na ingawa wewe ni mzeituni wa mwituni, ulipandikizwa kati yake na kuwa mshiriki wa utajiri wa mzizi wa mzeituni, 18 usijivune* dhidi ya matawi. Kama ukijivuna* dhidi yake,+ kumbuka kwamba, si wewe unayebeba mzizi, bali ni mzizi unaokubeba wewe. 19 Basi, utasema: “Matawi yalikatwa ili mimi nipandikizwe.”+ 20 Hilo ni kweli! Walikatwa+ kwa sababu walikosa imani, lakini wewe umesimama kwa imani.+ Usiwe na majivuno, bali uwe na woga. 21 Kwa maana ikiwa Mungu hakuyaacha matawi ya asili, vivyo hivyo hatakuacha wewe. 22 Kwa hiyo, fikiria fadhili+ na ukali wa Mungu. Kuna ukali kuwaelekea wale walioanguka,+ lakini kukuelekea wewe kuna fadhili za Mungu mradi tu ukae katika fadhili zake; la sivyo, wewe pia utakatwa. 23 Wao pia, ikiwa hawataendelea kukosa imani, watapandikizwa,+ kwa kuwa Mungu anaweza kuwapandikiza tena. 24 Kwa maana ikiwa wewe ulikatwa kutoka kwenye mzeituni wa mwituni na kupandikizwa kinyume cha asili kwenye mzeituni wa bustani, je, hawa walio wa asili hawatapandikizwa tena kwenye mzeituni wao wenyewe?
25 Kwa maana sitaki ninyi, akina ndugu, mkose kuijua siri hii takatifu,+ ili msiwe wenye hekima machoni penu wenyewe: Hisia za Israeli zimetiwa uzito kwa kiasi fulani mpaka idadi kamili ya watu wa mataifa itakapoingia, 26 na kwa njia hii Israeli wote+ wataokolewa. Kama ilivyoandikwa: “Mkombozi* atakuja kutoka Sayuni+ na kuondoa mazoea ya kutomwogopa Mungu kutoka katika Yakobo. 27 Na hili ndilo agano langu pamoja nao,+ nitakapoondoa dhambi zao.”+ 28 Ni kweli, kuhusu habari njema wao ni adui kwa ajili yenu, lakini kuhusu uchaguzi wa Mungu wao ni wapendwa kwa ajili ya mababu zao.+ 29 Kwa kuwa Mungu hataghairi kwa sababu ya zawadi na mwito anaotoa. 30 Kwa maana kama vile ninyi wakati fulani mlivyokuwa watu wasiomtii Mungu+ lakini sasa mmeonyeshwa rehema+ kwa sababu ya kutotii kwao,+ 31 ndivyo pia hawa sasa wamekuwa wasiotii na hivyo mkaonyeshwa rehema, ili wao wenyewe pia waonyeshwe rehema sasa. 32 Kwa maana Mungu amewaweka wote pamoja katika kutotii,+ ili awaonyeshe wote rehema.+
33 Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyochunguzika na njia zake zisivyotafutika! 34 Kwa maana “ni nani ameijua akili ya Yehova,* au ni nani amekuwa mshauri wake?”+ 35 Au, “Ni nani amempa yeye kwanza, hivi kwamba iwe lazima arudishiwe?”+ 36 Kwa sababu vitu vyote vimetoka kwake, kupitia yeye na kwa ajili yake. Kwake yeye na kuwe na utukufu milele. Amina.
12 Kwa hiyo akina ndugu, ninawasihi kwa huruma za Mungu, mtoe miili yenu+ iwe dhabihu iliyo hai, takatifu,+ na yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri.+ 2 Na acheni kufinyangwa na mfumo huu wa mambo,* bali mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu,+ ili mjihakikishie wenyewe+ mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.
3 Kwa maana kupitia fadhili zisizostahiliwa nilizopewa ninamwambia kila mtu kati yenu asijifikirie mwenyewe kuliko ilivyo lazima kufikiri,+ bali afikiri ili awe na akili timamu, kila mmoja kama Mungu alivyompa* kipimo cha imani.+ 4 Kwa maana kama vile tulivyo na viungo vingi katika mwili mmoja,+ lakini viungo hivyo havifanyi kazi ileile, 5 ndivyo sisi, ingawa tuko wengi, ni mwili mmoja katika muungano na Kristo, lakini kila mmoja wetu ni kiungo cha mwingine.+ 6 Basi, kwa kuwa tuna zawadi zinazotofautiana kulingana na fadhili zisizostahiliwa tulizopewa,+ kama ni ya unabii, na tutoe unabii kulingana na imani yetu; 7 au kama ni ya huduma, na tuwe katika huduma hii; au yule anayefundisha, na aendelee kufundisha;+ 8 au yule anayetia moyo,* na atie moyo;*+ yule anayegawa,* na afanye hivyo kwa ukarimu;+ yule anayesimamia,* na afanye hivyo kwa bidii;*+ yule anayeonyesha rehema, na afanye hivyo kwa uchangamfu.+
9 Upendo wenu na uwe bila unafiki.+ Chukieni maovu;+ shikamaneni na mema. 10 Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima, iweni wa kwanza.*+ 11 Iweni wenye bidii,* msiwe wavivu.*+ Wakeni roho.+ Mtumikieni Yehova.*+ 12 Shangilieni katika tumaini. Vumilieni chini ya dhiki.+ Dumuni katika sala.+ 13 Shirikini pamoja na watakatifu kulingana na mahitaji yao.+ Iweni wakaribishaji wageni.*+ 14 Endeleeni kuwabariki wale wanaowatesa;+ muwe mkibariki msiwe mkilaani.+ 15 Shangilieni na wale wanaoshangilia; lieni na wale wanaolia. 16 Wafikirieni wengine kama mnavyojifikiria; msikazie akili zenu kwenye mambo makuu,* bali mwongozwe na mambo ya hali ya chini.+ Msiwe wenye hekima machoni penu wenyewe.+
17 Msimlipe yeyote uovu kwa uovu.+ Zingatieni mambo yaliyo mema kulingana na maoni ya* watu wote. 18 Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, fanyeni amani na watu wote.+ 19 Wapendwa, msijilipizie kisasi bali iachieni nafasi ghadhabu;*+ kwa maana imeandikwa: “Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.”*+ 20 Lakini, “ikiwa adui yako ana njaa, mlishe; ikiwa ana kiu, mpe kitu anywe; kwa maana kwa kufanya hivyo utakusanya makaa ya mawe yanayowaka juu ya kichwa chake.”*+ 21 Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.+
13 Kila mtu na ajitiishe* kwa mamlaka zilizo kubwa,+ kwa maana hakuna mamlaka isipokuwa kupitia Mungu;+ mamlaka zilizopo zimewekwa na Mungu katika vyeo vyao vya kadiri.+ 2 Kwa hiyo, yeyote anayepinga mamlaka amechukua msimamo dhidi ya mpango wa Mungu; wale ambao wamechukua msimamo dhidi ya mpango huo, watajiletea hukumu wao wenyewe. 3 Kwa maana watawala ni kitu cha kuogopesha, si kwa tendo jema, bali kwa baya.+ Je, unataka usiogope hiyo mamlaka? Endelea kufanya mema,+ nayo itakusifu; 4 kwa maana hiyo ni mhudumu wa Mungu kwako kwa faida yako. Lakini ikiwa unafanya mabaya, ogopa, kwa maana haichukui upanga bila kusudi. Hiyo ni mhudumu wa Mungu, nayo hulipiza kisasi ili kuonyesha ghadhabu* dhidi ya yule anayefanya mabaya.
5 Kwa hiyo kuna sababu ya lazima kwenu kujitiisha, si kwa sababu ya ghadhabu hiyo tu, bali pia kwa sababu ya dhamiri yenu.+ 6 Ndiyo maana mnalipa kodi pia; kwa kuwa wao ni watumishi wa Mungu kwa watu wote wakitumikia daima kwa kusudi hili. 7 Wapeni wote haki zao: yule anayetaka kodi, kodi;+ yule anayetaka ushuru, ushuru; yule anayetaka woga, woga huo;+ yule anayetaka heshima, heshima hiyo.+
8 Msiwe na deni lolote kwa mtu yeyote, isipokuwa kupendana,+ kwa maana yeyote anayempenda mwanadamu mwenzake ameitimiza sheria.+ 9 Kwa maana sheria zinazosema, “Usifanye uzinzi,+ usiue,+ usiibe,+ usitamani,”+ na amri nyingine yoyote iliyopo, zimejumlishwa katika maneno haya: “Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.”+ 10 Upendo haumfanyii uovu jirani;+ kwa hiyo, upendo ndio utimizo wa sheria.+
11 Nanyi fanyeni hivi kwa sababu mnayajua majira, kwamba tayari ni saa yenu ya kuamka kutoka usingizini,+ kwa maana sasa wokovu wetu uko karibu zaidi kuliko wakati tulipoanza kuamini. 12 Usiku umesonga sana; mchana umekaribia. Kwa hiyo, na tuyaache matendo ya giza+ na tuvae silaha za nuru.+ 13 Na tujiendeshe kwa adabu+ kama wakati wa mchana, si katika karamu zenye vurugu* na ulevi, si katika ngono isiyo halali na mwenendo mpotovu,*+ si katika mizozo na wivu.+ 14 Bali mvaeni Bwana Yesu Kristo,+ na msiwe mkipanga mapema kwa ajili ya tamaa za mwili.+
14 Mkaribisheni mtu aliye na udhaifu katika imani yake,+ lakini msihukumu kuhusu maoni yanayotofautiana.* 2 Mtu mmoja ana imani ya kula kila kitu, lakini mtu aliye dhaifu hula mboga za majani tu. 3 Yule anayekula asimdharau yule asiyekula, na yule asiyekula asimhukumu yule anayekula,+ kwa maana Mungu amemkaribisha. 4 Wewe ni nani ili umhukumu mtumishi wa mwingine?+ Kwa bwana wake yeye husimama au kuanguka.+ Kwa kweli, atasimamishwa, kwa maana Yehova* anaweza kumsimamisha.
5 Mtu mmoja anahukumu siku moja kuwa muhimu kuliko nyingine;+ mwingine anahukumu siku moja kuwa sawa na nyingine zote;+ kila mtu na asadikishwe kikamili katika akili yake mwenyewe. 6 Yule anayeishika siku huishika kwa ajili ya Yehova.* Pia, yule anayekula, anakula kwa ajili ya Yehova,* kwa maana yeye humshukuru Mungu;+ na yule asiyekula, hali chakula kwa ajili ya Yehova,* na bado yeye humshukuru Mungu.+ 7 Hakuna hata mmoja wetu anayeishi kwa ajili yake mwenyewe tu,+ na hakuna yeyote anayekufa kwa ajili yake mwenyewe tu. 8 Kwa maana tukiishi, tunaishi kwa ajili ya Yehova,*+ na tukifa, tunakufa kwa ajili ya Yehova.* Basi tukiishi na tukifa, sisi ni wa Yehova.*+ 9 Kwa maana kwa kusudi hili Kristo alikufa na akawa hai tena, ili awe Bwana juu ya waliokufa na walio hai pia.+
10 Lakini kwa nini unamhukumu ndugu yako?+ Au kwa nini pia unamdharau ndugu yako? Kwa maana sisi sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu.+ 11 Kwa maana imeandikwa: “‘Kwa hakika kama ninavyoishi,’+ asema Yehova,* ‘kila goti litapigwa mbele zangu, na kila ulimi utakiri waziwazi kwa Mungu.’”+ 12 Hivyo basi, kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.+
13 Kwa hiyo tusiwe tukihukumiana tena,+ badala yake tuazimie kutoweka kikwazo au kizuizi mbele ya ndugu.+ 14 Ninajua, nami ninaamini katika Bwana Yesu kwamba hakuna kitu ambacho ndani yake chenyewe ni kichafu;+ isipokuwa tu mtu anapokiona kitu kuwa kichafu, kwake yeye hicho huwa kichafu. 15 Kwa maana ikiwa unamkasirisha ndugu yako kwa sababu ya chakula, wewe hutembei tena kulingana na upendo.+ Kwa chakula chako usimwangamize* yule ambaye Kristo alikufa kwa ajili yake.+ 16 Kwa hiyo, msiache mema mnayofanya yasemwe vibaya. 17 Kwa maana Ufalme wa Mungu haumaanishi kula na kunywa,+ bali unamaanisha uadilifu na amani na shangwe pamoja na roho takatifu. 18 Kwa maana yeyote anayemtumikia Kristo kwa njia hii anakubalika kwa Mungu naye ana kibali cha wanadamu.
19 Hivyo basi, na tufuatilie mambo yanayoleta amani+ na mambo ya kujengana.+ 20 Acheni kuibomoa kazi ya Mungu kwa ajili ya chakula tu.+ Ni kweli, vitu vyote ni safi, lakini ni vibaya* kwa mtu kula ikiwa itasababisha kikwazo.+ 21 Ni vema kutokula nyama au kunywa divai au kufanya jambo lolote ambalo litamkwaza ndugu yako.+ 22 Imani uliyo nayo, endelea kuwa nayo mbele za Mungu. Mwenye furaha ni mtu asiyejihukumu mwenyewe kwa yale anayokubali. 23 Lakini ikiwa ana shaka, yeye akila tayari atakuwa amehukumiwa kuwa mwenye hatia, kwa sababu hali kwa imani. Kwa kweli, kila kitu ambacho hakitokani na imani ni dhambi.
15 Basi, sisi tulio na nguvu tunapaswa kubeba udhaifu wa wale wasio na nguvu,+ na tusiwe tukijipendeza wenyewe.+ 2 Kila mmoja wetu na ampendeze jirani yake kwa mema, ili kumjenga.+ 3 Kwa maana hata Kristo hakujipendeza mwenyewe,+ bali kama ilivyoandikwa: “Shutuma za wale wanaokushutumu zimeniangukia.”+ 4 Kwa maana mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha,+ ili kupitia uvumilivu wetu+ na kupitia faraja kutoka kwa Maandiko tuwe na tumaini.+ 5 Basi Mungu anayetoa uvumilivu na faraja na awawezeshe ninyi miongoni mwenu wenyewe kuwa na mtazamo uleule wa akili ambao Kristo Yesu alikuwa nao, 6 ili kwa umoja+ na kwa sauti moja* mumtukuze Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo.
7 Basi mkaribishane,*+ kama vile Kristo pia alivyowakaribisha,+ kwa kusudi la kumtukuza Mungu. 8 Kwa maana ninawaambia kwamba Kristo alikuwa mhudumu wa wale waliotahiriwa+ kwa ajili ya ukweli wa Mungu, ili kuthibitisha ahadi ambazo Yeye aliwapa mababu zao,+ 9 na kwamba mataifa yamtukuze Mungu kwa sababu ya rehema yake.+ Kama ilivyoandikwa: “Ndiyo sababu nitakukiri wewe waziwazi kati ya mataifa nami nitakwimbia nyimbo za sifa.”+ 10 Tena anasema: “Furahini, enyi mataifa, pamoja na watu wake.”+ 11 Tena: “Msifuni Yehova,* enyi mataifa yote, na watu wote wamsifu yeye.”+ 12 Na tena Isaya anasema: “Kutakuwa na mzizi wa Yese,+ yule anayesimama ili kutawala mataifa;+ na mataifa yatamtumainia yeye.”+ 13 Mungu anayetoa tumaini na awajaze ninyi shangwe yote na amani kwa kumtegemea, ili tumaini lenu liongezeke* kwa nguvu za roho takatifu.+
14 Ndugu zangu, sasa mimi mwenyewe nimesadiki kuwahusu, kwamba ninyi pia mmejaa wema, mmejaa ujuzi wote, na kwamba mnaweza kuonyana.* 15 Hata hivyo, nimewaandikia waziwazi zaidi kuhusu mambo fulani, ili kuwakumbusha tena, kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa nilizopewa kutoka kwa Mungu 16 ili niwe mtumishi wa watu wote wa Kristo Yesu kwa mataifa.+ Ninafanya kazi takatifu ya habari njema ya Mungu,+ ili mataifa haya yawe toleo linalokubalika, lililotakaswa kwa roho takatifu.
17 Basi nina sababu ya kufurahi katika Kristo Yesu kuhusu mambo yanayohusiana na Mungu. 18 Kwa maana sitathubutu kusema kuhusu chochote isipokuwa yale ambayo Kristo amefanya kupitia mimi ili mataifa yatii, kwa maneno na matendo yangu, 19 kwa nguvu za ishara na mambo ya ajabu,*+ kwa nguvu za roho ya Mungu, hivi kwamba kutoka Yerusalemu na kuzunguka mpaka Ilirikamu nimehubiri kikamili habari njema kuhusu Kristo.+ 20 Kwa kweli, katika njia hii, nilikusudia kwamba nisitangaze habari njema mahali ambapo jina la Kristo lilikuwa limetangazwa tayari, ili nisijenge juu ya msingi wa mtu mwingine; 21 bali, kama ilivyoandikwa: “Wale ambao hawajapata ujumbe wowote kumhusu wataona, na wale ambao hawajasikia wataelewa.”+
22 Pia hiyo ndiyo sababu nilizuiwa mara nyingi kuja kwenu. 23 Lakini sasa sina tena eneo ambalo halijaguswa katika maeneo haya, na kwa miaka mingi* nimetamani kuja kwenu. 24 Kwa hiyo, nikisafiri kwenda Uhispania, natumaini kwamba nitawaona na mtanisindikiza umbali fulani, baada ya mimi kufurahia ushirika wenu kwa muda. 25 Lakini sasa ninakaribia kusafiri kwenda Yerusalemu kuwahudumia watakatifu.+ 26 Kwa maana wale walio Makedonia na Akaya wamependezwa kushiriki vitu vyao kwa kuwatolea mchango fulani walio maskini kati ya watakatifu huko Yerusalemu.+ 27 Kweli, wamependezwa kufanya hivyo, na kwa hakika walikuwa wadeni kwao; kwa maana ikiwa mataifa wameshiriki mambo yao ya kiroho, wao pia wana deni la kuwahudumia kwa vitu vyao vya kimwili.+ 28 Basi nikimaliza jambo hili na kuwafikishia mchango huu* salama, nitaondoka na kupitia kwenu nikielekea Uhispania. 29 Isitoshe, najua kwamba nitakapokuja kwenu nitakuja nikiwa na kipimo kamili cha baraka kutoka kwa Kristo.
30 Sasa ninawahimiza ninyi, akina ndugu, kupitia Bwana wetu Yesu Kristo na kupitia upendo wa roho, kwamba mjikaze pamoja nami katika kusali kwa Mungu kwa ajili yangu,+ 31 ili nikombolewe+ kutoka kwa wale wasio waamini huko Yudea na kwamba huduma yangu kwa ajili ya Yerusalemu ikubalike kwa watakatifu,+ 32 ili kwa mapenzi ya Mungu nije kwenu nikiwa na shangwe na kuburudishwa pamoja nanyi. 33 Mungu anayetoa amani na awe pamoja nanyi nyote.+ Amina.
16 Ninamtambulisha* kwenu Fibi dada yetu, ambaye ni mhudumu wa kutaniko lililo huko Kenkrea,+ 2 ili mumkaribishe katika Bwana kwa njia inayowastahili watakatifu, na kumpa msaada wowote ambao huenda akahitaji,+ kwa maana yeye pia alikuwa mtetezi wa wengi, kutia ndani mimi mwenyewe.
3 Wapeni salamu zangu Priska na Akila,+ wafanyakazi wenzangu katika Kristo Yesu, 4 ambao wamehatarisha shingo zao kwa ajili yangu,*+ na si mimi tu ninayewashukuru bali pia makutaniko yote ya mataifa. 5 Pia salimuni kutaniko lililo katika nyumba yao.+ Msalimuni Epaineto mpendwa wangu, aliye matunda ya kwanza ya Asia kwa ajili ya Kristo. 6 Msalimuni Maria, ambaye amefanya kazi kwa bidii kwa ajili yenu. 7 Wasalimuni Androniko na Yunia, watu wangu wa ukoo+ na wafungwa wenzangu, ambao ni watu wanaojulikana kwa mitume na ambao wamekuwa katika muungano na Kristo muda mrefu zaidi yangu.
8 Mpeni salamu zangu Ampliato, mpendwa wangu katika Bwana. 9 Salimuni Urbano mfanyakazi mwenzetu katika Kristo, na Stako mpendwa wangu. 10 Msalimuni Apele, aliyekubaliwa katika Kristo. Wasalimuni wale wa nyumbani mwa Aristobulo. 11 Msalimuni Herodioni, mtu wangu wa ukoo. Wasalimuni wale wa nyumbani mwa Narkiso walio katika Bwana. 12 Wasalimuni Trifaina na Trifosa, wanawake wanaofanya kazi kwa bidii katika Bwana. Msalimuni Persisi mpendwa wetu, kwa maana mwanamke huyo amefanya kazi kwa bidii katika Bwana. 13 Salimuni Rufo aliyechaguliwa katika Bwana, na mama yake ambaye pia ni mama yangu. 14 Wasalimuni Asinkrito, Flegoni, Hermesi, Patroba, Hermasi, na akina ndugu walio pamoja nao. 15 Wasalimuni Filologo na Yulia, Nerea na dada yake, na Olimpa, na watakatifu wote walio pamoja nao. 16 Salimianeni kwa busu takatifu. Makutaniko yote ya Kristo yanawasalimu ninyi.
17 Sasa ninawahimiza ninyi, akina ndugu, waangalieni wale wanaosababisha migawanyiko na kuweka vikwazo kinyume cha fundisho ambalo mmejifunza, nanyi mjiepushe nao.+ 18 Kwa maana watu wa namna hiyo ni watumwa, si wa Bwana wetu Kristo, bali wa hamu* yao wenyewe, na kwa maneno laini na maneno ya kusifusifu wao huishawishi mioyo ya wasiotambua. 19 Utii wenu umejulikana na watu wote, basi ninashangilia kwa sababu yenu. Hata hivyo, ninataka muwe na hekima kuhusu yaliyo mema, lakini wasio na hatia kuhusu yaliyo maovu.+ 20 Kwa upande wake, Mungu anayetoa amani atamponda Shetani+ chini ya miguu yenu hivi karibuni. Fadhili zisizostahiliwa za Bwana wetu Yesu na ziwe pamoja nanyi.
21 Timotheo, mfanyakazi mwenzangu anawasalimu ninyi, na pia Lukio, Yasoni, na Sosipata, watu wangu wa ukoo.+
22 Mimi, Tertio, ambaye nimeiandika barua hii, ninawasalimu ninyi katika Bwana.
23 Gayo,+ aliyenikaribisha mimi na kutaniko lote, anawasalimu ninyi. Erasto, mweka hazina* wa jiji, anawasalimu ninyi, na pia Kwarto, ndugu yake. 24* ——
25 Sasa kwa Yule anayeweza kuwaimarisha ninyi kulingana na habari njema ninayotangaza na kuhubiriwa kwa Yesu Kristo, kulingana na ufunuo wa siri takatifu+ ambayo ilikuwa imefichwa tangu nyakati za zamani 26 lakini sasa imeonyeshwa wazi* na kujulishwa kupitia Maandiko ya kinabii kati ya mataifa yote kulingana na amri ya Mungu anayedumu milele, ili kuendeleza utii kwa imani; 27 kwa Mungu, ambaye peke yake ndiye mwenye hekima,+ kuwe na utukufu kupitia Yesu Kristo milele. Amina.
Tnn., “mbegu ya.”
Au “kuwe na ubadilishanaji wa kitia moyo.”
Au “wasio Wagiriki.” Tnn., “wabaribari.”
Au “kufa.”
Au “wakauheshimu sana.”
Au “mahusiano ya asili pamoja na.”
Au “malipo.”
Au “hawakukubali kumjua Mungu katika ujuzi sahihi.”
Au “tamaa mbaya.”
Au “wadaku; wambeya.”
Au “yenye kudhuru.”
Au “ustahimilivu.”
Au “nafsi ya kila mtu.”
Tnn., “katikati ya.”
Au “unafundishwa kwa mdomo.”
Tnn., “mwili wowote utakaotangazwa.”
Au “dhabihu ya kufunika dhambi.”
Au “ustahimilivu.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “zimesamehewa.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “dhamana ya; uhakikisho wa.”
Tnn., “mbegu yake.”
Tnn., “mbegu yake.”
Au labda, “anafanya vitu visivyokuwapo viwepo.”
Tnn., “mbegu yako.”
Au “hali ya kuwa tasa.”
Au labda, “tuna amani.”
Au labda, “tunashangilia.”
Au labda, “tunashangilia.”
Au “zilifurika.”
Au “amefunguliwa; amesamehewa.”
Yaani, kuondoa dhambi.
Tnn., “viungo vyenu.”
Tnn., “viungo vyenu.”
Tnn., “viungo vyetu.”
Tnn., “viungo vyangu.”
Tnn., “viungo vyangu.”
Neno la Kiebrania au Kiaramu linalomaanisha “Ee Baba!”
Au “kusikosemwa.”
Tnn., “mbegu ya.”
Tnn., “mbegu yako.”
Tnn., “mbegu.”
Tnn., “yule anayetaka wala yule anayekimbia.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “kuifanya haraka.”
Angalia Nyongeza A5.
Tnn., “mbegu.”
Au “anayeonyesha imani.”
Au “abiso.” Angalia Kamusi.
Au “mkarimu.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Au “ujumbe wetu.”
Tnn., “mbegu ya.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “kuchukua uhai (nafsi) wangu.”
Au “ninaisifu.”
Tnn., “mwili wangu uwe.”
Au “usijigambe.”
Au “ukijigamba.”
Au “Mwokozi.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Au “alivyomgawia.”
Au “anayehimiza.”
Au “ahimize.”
Au “anayechangia.”
Au “anayeongoza.”
Au “juhudi.”
Au “chukueni hatua ya kwanza.”
Au “jitihada.”
Au “msiwe wavivu katika kazi zenu.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “iweni wakarimu.”
Au “msifikirie makuu.”
Au “machoni pa.”
Yaani, ghadhabu ya Mungu.
Angalia Nyongeza A5.
Yaani, kupunguza uadui wake na kuyeyusha ugumu wake.
Au “Kila nafsi na ijitiishe.”
Au “kuleta adhabu.”
Au “karamu za kupindukia.”
Au “ufidhuli; matendo ya kuchukiza yanayofanywa bila aibu.” Wingi wa neno la Kigiriki a·selʹgei·a. Angalia Kamusi.
Au labda, “maswali ya ndani.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Au “usimharibu.”
Au “kosa.”
Tnn., “kinywa kimoja.”
Au “muwakubali wengine.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “lifurike.”
Au “kufundishana.”
Au “miujiza.”
Au labda, “kadhaa.”
Tnn., “tunda hili.”
Au “Ninampendekeza.”
Au “nafsi yangu.”
Au “matumbo.”
Au “msimamizi.”
Angalia Nyongeza A3.
Au “imefunuliwa.”