Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • bi12 Esta 1:1-10:3
  • Esta

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Esta
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Esta

Esta

1 Basi ikatokea katika siku za Ahasuero,+ yaani, yule Ahasuero aliyekuwa akitawala akiwa mfalme kutoka India mpaka Ethiopia, juu ya wilaya za utawala 127,+ 2 kwamba katika siku hizo Mfalme Ahasuero alipokuwa anaketi juu ya kiti chake cha ufalme,+ kilichokuwa katika ngome+ ya Shushani,+ 3 katika mwaka wa tatu wa utawala wake alifanya karamu+ kwa ajili ya wakuu wake na watumishi wake wote, jeshi la Uajemi+ na Umedi,+ watu wenye vyeo+ na kwa ajili ya wakuu wa wilaya za utawala mbele yake.+ 4 Ndipo akaonyesha utajiri+ wa ufalme wake wenye utukufu, na heshima+ na uzuri wa ukuu wake kwa muda wa siku nyingi, siku 180. 5 Hata siku hizo zilipotimia, kwa siku saba mfalme akawafanyia karamu watu wote waliokuwa katika ngome ya Shushani, wakubwa kwa wadogo, katika ua wa bustani ya jumba la kifalme. 6 Kulikuwa na vitambaa vya kitani, vya pamba bora na bluu+ vimefungwa imara katika kamba za kitambaa laini, na sufu iliyotiwa rangi ya zambarau+ katika pete za fedha na nguzo za marumaru, vitanda+ vya dhahabu na fedha juu ya sakafu ya mawe mekundu na marumaru na lulu na marumaru nyeusi.

7 Na divai ya kunywa ikapitishwa katika vyombo vya dhahabu;+ na vyombo hivyo vilikuwa vya aina mbalimbali, na divai ya kifalme+ ilikuwa nyingi sana, kulingana na mali ya mfalme. 8 Na kuhusu wakati wa kunywa kulingana na sheria, hakuna aliyekuwa akilazimishwa, kwa maana hivyo ndivyo mfalme alivyokuwa amepangia kila mtu mkuu katika nyumba yake, kila mtu atende kama anavyopenda.

9 Pia, Vashti,+ malkia, akawafanyia wanawake karamu katika nyumba ya kifalme ya Mfalme Ahasuero.

10 Siku ya saba, moyo wa mfalme ulipokuwa umechangamshwa na divai,+ aliwaambia Mehumani, Biztha, Harbona,+ Bigtha na Abagtha, Zethari na Karkasi, wale maofisa saba wa makao ya mfalme waliokuwa wakihudumu+ mbele ya Mfalme Ahasuero, 11 wamlete Vashti, malkia, mbele ya mfalme, akiwa na taji la kifalme, ili awaonyeshe vikundi vya watu na wakuu uzuri wake; kwa maana alikuwa mrembo.+ 12 Lakini Malkia Vashti akazidi kukataa+ kuja kufuatia agizo la mfalme kwa mkono wa maofisa wa makao ya mfalme. Kwa hiyo mfalme akaudhika sana na ghadhabu yake ikawaka ndani yake.+

13 Na mfalme akawaambia watu wenye hekima+ walio na ujuzi wa nyakati+ (kwa maana hivyo ndivyo mambo ya mfalme yalivyokuja mbele ya wote wenye ujuzi wa sheria na kesi. 14 Na wale waliokuwa karibu zaidi naye ni Karshena, Shethari, Admatha, Tarshishi, Meresi, Marsena, na Memukani, wakuu saba+ wa Uajemi na Umedi, wanaoingia kwa mfalme,+ nao walikuwa wanaketi katika cheo cha kwanza katika ufalme): 15 “Kulingana na sheria, Malkia Vashti afanyiwe nini kwa sababu hakutenda neno la Mfalme Ahasuero lililotolewa kupitia maofisa wa makao ya mfalme?”

16 Memukani+ akajibu na kusema mbele ya mfalme na wakuu: “Huyu Vashti, malkia, hakufanya kosa juu ya mfalme peke yake,+ bali pia juu ya wakuu wote na vikundi vyote vya watu walioko katika wilaya zote za utawala za Mfalme Ahasuero. 17 Maana tendo hili la malkia litawafikia wake wote nao watawadharau+ waume+ zao machoni pao, wanaposema, ‘Mfalme Ahasuero alisema Vashti, malkia, aingizwe ndani mbele yake, naye hakuingia ndani.’ 18 Na leo binti za kifalme wa Uajemi na Umedi, ambao wamesikia juu ya tendo hilo la malkia, watawaambia wakuu wote wa mfalme, na kutakuwa na dharau na ghadhabu tele.+ 19 Mfalme akiona vema,+ na litoke kwake neno la kifalme, nalo liandikwe kati ya sheria+ za Uajemi na Umedi, ili lisipitilie mbali,+ kwamba Vashti asije mbele ya Mfalme Ahasuero; na heshima yake ya kifalme mfalme ampe mmoja wa wenzake, mwanamke aliye bora kuliko yeye. 20 Na amri atakayotoa mfalme itangazwe katika utawala wake wote (maana ni mkubwa sana), na wake wote watawapa waume+ zao heshima,+ wakubwa kwa wadogo.”

21 Na jambo hilo likapendeza machoni pa mfalme+ na wakuu, naye mfalme akafanya kulingana na neno la Memukani. 22 Basi akatuma barua+ kwa wilaya zote za utawala wa mfalme, kwa kila wilaya+ kwa mtindo wake wa kuandika na kwa kila kikundi cha watu kwa lugha yao, kwamba kila mume aendelee kuwa mkuu nyumbani mwake+ na kusema kwa lugha ya watu wake mwenyewe.

2 Baada ya mambo hayo, ghadhabu ya Mfalme Ahasuero+ ilipopungua, alimkumbuka Vashti+ pamoja na kile alichofanya+ na yale yaliyoamuliwa juu yake.+ 2 Ndipo watumishi wa mfalme, wahudumu wake,+ wakasema: “Na wamtafutie+ mfalme wanawake vijana, mabikira,+ warembo. 3 Naye mfalme achague wajumbe katika wilaya+ zote za utawala katika milki yake, nao wakusanye pamoja katika ngome+ ya Shushani wanawake wote vijana, mabikira, warembo, kwenye nyumba ya wanawake chini ya Hegai+ towashi+ wa mfalme, mlinzi wa wanawake; nao wakandwe. 4 Na yule mwanamke kijana atakayeonekana kuwa anapendeza machoni pa mfalme atakuwa malkia badala ya Vashti.”+ Na jambo hilo likapendeza machoni pa mfalme, naye akafanya hivyo.

5 Mwanamume fulani, Myahudi, alikuwa katika ngome ya Shushani,+ jina lake lilikuwa Mordekai+ mwana wa Yairi mwana wa Shimei mwana wa Kishi, Mbenyamini,+ 6 aliyekuwa amepelekwa uhamishoni+ kutoka Yerusalemu pamoja na watu waliohamishwa ambao walipelekwa uhamishoni pamoja na Yekonia+ mfalme wa Yuda ambaye Nebukadneza+ mfalme wa Babiloni alimpeleka uhamishoni. 7 Naye akawa mlezi+ wa Hadasa, yaani, Esta, binti ya ndugu ya baba yake,+ kwa maana hakuwa na baba wala mama. Na huyo mwanamke kijana alikuwa mrembo na mwenye umbo linalopendeza,+ na wakati baba na mama yake walipokufa, Mordekai alimchukua awe binti yake. 8 Kisha ikatukia kwamba, wakati neno la mfalme na sheria yake iliposikiwa, na wanawake wengi vijana walipokusanywa pamoja kwenye ngome ya Shushani+ chini ya Hegai,+ Esta naye alipelekwa katika nyumba ya mfalme chini ya Hegai mlinzi wa wanawake.

9 Basi huyo mwanamke kijana akawa mwenye kupendeza machoni pake, akapata fadhili zenye upendo+ mbele yake, akafanya haraka kumpa vifaa vya kukandia+ na chakula chake kinachostahili, na kumpa wanawake vijana saba waliochaguliwa kutoka katika nyumba ya mfalme. Naye akamhamisha yeye na wale vijana wake mpaka mahali palipo bora zaidi nyumbani mwa wanawake. 10 Esta hakuwa amesema kuhusu watu wake+ wala kuhusu jamaa zake, kwa maana Mordekai alikuwa amemwamuru kwamba asiseme.+ 11 Na Mordekai akawa akitembea siku baada ya siku mbele ya ua wa nyumba ya wanawake, apate kujua hali ya Esta na mambo waliyokuwa wakimtendea.

12 Zamu ya kila mwanamke kijana ilipofika ya kuingia kwa Mfalme Ahasuero baada ya kufanyiwa kulingana na masharti ya wanawake kwa miezi kumi na miwili, maana hivyo ndivyo hatua kwa hatua siku za utaratibu wao wa kukandwa zilivyotimia, miezi sita kwa mafuta ya manemane+ na miezi sita kwa mafuta ya zeri+ pamoja na kukandwa kwa wanawake; 13 ndipo kwa masharti haya kila mwanamke kijana alikuwa akiingia kwa mfalme. Naye alipewa kila kitu ambacho alitaka, ili atoke nacho katika nyumba ya wanawake kwenda katika nyumba ya mfalme.+ 14 Jioni alikuwa akiingia, na asubuhi alikuwa akirudi katika nyumba ya pili ya wanawake iliyosimamiwa na Shaashgazi towashi wa mfalme,+ mlinzi wa masuria. Hakuwa akiingia tena kwa mfalme ila mfalme awe alipendezwa naye na aitwe kwa jina lake.+

15 Zamu ya Esta binti ya Abihaili ndugu ya baba ya Mordekai, ambaye alikuwa amemchukua awe binti yake,+ ilipofika kuingia kwa mfalme, hakuomba chochote+ ila vile vitu ambavyo Hegai+ towashi wa mfalme, mlinzi wa wanawake, alitaja (wakati huo wote Esta alikuwa akizidi kupata kibali machoni pa kila mtu aliyemwona).+ 16 Ndipo Esta akapelekwa kwa Mfalme Ahasuero katika nyumba yake ya kifalme mwezi wa kumi, yaani, mwezi wa Tebethi, katika mwaka wa saba+ wa utawala wake. 17 Naye mfalme akampenda Esta kuliko wale wanawake wengine wote, hata akapata kibali na fadhili zenye upendo kuliko wale mabikira wengine wote.+ Ndipo mfalme akamvika taji la kifalme juu ya kichwa chake na kumfanya kuwa malkia+ badala ya Vashti. 18 Kisha mfalme akawafanyia karamu kubwa wakuu wake wote na watumishi wake, yaani, karamu yake Esta; akatoa msamaha+ kwa wilaya zake za utawala, naye akatoa zawadi kulingana na mali ya mfalme.

19 Basi mabikira+ walipokusanywa pamoja mara ya pili, Mordekai alikuwa ameketi katika lango la mfalme.+ 20 Esta hakuwa akisema kuhusu jamaa zake wala watu wake,+ kama Mordekai+ alivyokuwa amemwamuru;+ naye Esta alikuwa anashika neno la Mordekai, kama alivyokuwa akifanya akiwa chini ya ulezi wake.+

21 Siku hizo Mordekai alipokuwa anaketi katika lango la mfalme, Bigthani na Tereshi, maofisa wawili wa makao ya mfalme, watunza-milango, waligadhibika nao wakazidi kutafuta kumdhuru+ Mfalme Ahasuero. 22 Mordekai akapata kulijua jambo hilo, naye bila kukawia akamwambia+ Esta, malkia. Esta naye akasema na mfalme katika jina la Mordekai.+ 23 Ndipo jambo hilo likachunguzwa na kujulikana mwishowe, na wote wawili wakatundikwa+ juu ya mti;+ kisha hayo yakaandikwa katika kitabu cha mambo+ ya siku mbele ya mfalme.

3 Baada ya mambo hayo Mfalme Ahasuero alimtukuza Hamani+ mwana wa Hamedatha Mwagagi,+ akamwinua+ na kukiweka kiti chake juu ya wakuu wengine wote waliokuwa pamoja naye.+ 2 Na watumishi wote wa mfalme waliokuwa katika lango la mfalme+ walikuwa wanainama na kumsujudia Hamani, kwa maana mfalme alikuwa ametoa amri hiyo kumhusu. Lakini Mordekai hakuinama wala kusujudu.+ 3 Basi watumishi wa mfalme waliokuwa katika lango la mfalme wakaanza kumwambia Mordekai: “Kwa nini unavunja amri ya mfalme?”+ 4 Ikawa, waliposema naye siku baada ya siku naye hakuwasikiliza, wakamwambia Hamani ili kuona kama mambo yake Mordekai yangevumiliwa;+ maana alikuwa amewaambia kuwa yeye ni Myahudi.+

5 Basi Hamani akazidi kuona kwamba Mordekai hakuwa akiinama wala kumsujudia,+ naye Hamani akajawa na ghadhabu.+ 6 Lakini lilikuwa jambo la kudharaulika machoni pake kunyoosha mkono wake juu ya Mordekai peke yake, kwa maana walikuwa wamemwambia kuhusu watu wa Mordekai; kwa hiyo Hamani akaanza kutafuta kuwaangamiza+ Wayahudi wote waliokuwa katika utawala wote wa Ahasuero, watu wa Mordekai.+

7 Katika mwezi wa kwanza,+ yaani, mwezi wa Nisani, katika mwaka wa kumi na mbili+ wa Mfalme Ahasuero, mtu fulani alipiga Puri,+ yaani, Kura,+ mbele ya Hamani siku baada ya siku na mwezi baada ya mwezi, mpaka mwezi wa kumi na mbili, yaani, mwezi wa Adari.+ 8 Ndipo Hamani akamwambia Mfalme Ahasuero: “Kuna kikundi fulani cha watu waliotawanyika+ na kujitenga kati ya vikundi vya watu katika wilaya zote za utawala wako;+ na sheria zao ni tofauti na zile za watu wengine wote, nao hawatendi sheria za mfalme,+ na haifai kwa mfalme kuwaachilia. 9 Mfalme akiona vema, na iandikwe kwamba waharibiwe; nami nitalipa talanta elfu kumi+ za fedha mikononi mwa wale wanaofanya kazi+ hiyo kwa kuzileta katika hazina ya mfalme.”

10 Kwa hiyo mfalme akavua pete yake ya muhuri+ kutoka mkononi mwake na kumpa Hamani+ mwana wa Hamedatha Mwagagi,+ yule mwenye kuwaonyesha Wayahudi uadui.+ 11 Tena mfalme akamwambia Hamani: “Umepewa fedha,+ pia watu, ili uwafanyie kulingana na yaliyo mema machoni pako mwenyewe.”+ 12 Ndipo waandishi+ wa mfalme wakaitwa katika mwezi wa kwanza siku ya kumi na tatu ya mwezi huo. Basi kuandika+ kukaendelea kulingana na yote ambayo Hamani aliwaamuru maliwali wa mfalme na magavana waliokuwa juu ya wilaya mbalimbali za utawala,+ na wakuu wa vikundi mbalimbali vya watu, wa kila wilaya ya utawala, katika mtindo wao wa kuandika,+ na kila kikundi cha watu kwa lugha yao wenyewe. Hayo yaliandikwa kwa jina+ la Mfalme Ahasuero na kutiwa muhuri kwa pete+ ya mfalme.

13 Na barua zikapelekwa kwa mkono wa wajumbe+ kwa wilaya zote za utawala wa mfalme, ili kuangamiza, kuua na kuharibu Wayahudi wote, vijana kwa wazee, watoto kwa wanawake, katika siku moja,+ siku ya kumi na tatu ya mwezi wa kumi na mbili, yaani, mwezi wa Adari,+ na kuteka nyara na kuwapora.+ 14 Nakala ya maandishi hayo, iliyopaswa kutolewa iwe sheria+ katika wilaya zote mbalimbali za utawala+ ilikuwa ikitangaziwa vikundi vyote vya watu, ili wawe tayari kwa siku hiyo. 15 Wajumbe hao wakaondoka, wakaenda haraka+ kwa sababu ya neno la mfalme, na sheria hiyo ikatolewa katika ngome ya Shushani.+ Naye mfalme pamoja na Hamani wakaketi ili kunywa;+ bali jiji la Shushani+ likavurugika.+

4 Basi Mordekai+ akapata kujua mambo yote yaliyokuwa yamefanywa;+ ndipo Mordekai akararua mavazi yake na kuvaa nguo za magunia+ na majivu,+ akaenda katikati ya jiji, akalia kwa sauti kubwa na yenye uchungu.+ 2 Mwishowe akaja mpaka mbele ya lango la mfalme,+ kwa maana hakuna yeyote aliyepaswa kuingia katika lango la mfalme akiwa amevaa nguo za magunia. 3 Na katika wilaya zote mbalimbali za utawala,+ kokote ambako neno la mfalme na sheria yake ilikuwa ikifika, kulitokea maombolezo+ makubwa kati ya Wayahudi, na kufunga,+ na kulia, na kuomboleza. Na wengi wakatandika nguo za magunia+ na majivu+ kuwa vitanda vyao. 4 Na wanawake vijana wa Esta na matowashi+ wake wakaingia na kumpa habari. Na malkia akaumia sana. Kisha akaagiza mavazi ya kumvika Mordekai yapelekwe na nguo zake za magunia zivuliwe. Naye hakuyakubali.+ 5 Kisha Esta akamwita Hathaki,+ mmoja wa matowashi wa mfalme, ambaye mfalme alikuwa amemweka amhudumie Esta, akampa amri kumhusu Mordekai, apate kuyajua mambo hayo na maana yake.

6 Basi Hathaki akaenda kwa Mordekai kwenye kiwanja cha watu wote cha jiji kilichokuwa mbele ya lango la mfalme. 7 Ndipo Mordekai akamweleza kuhusu mambo yote yaliyompata+ na taarifa kamili ya pesa ambazo Hamani alikuwa amesema atalipa kwa hazina+ ya mfalme juu ya Wayahudi, ili kuwaangamiza.+ 8 Naye akampa nakala+ ya maandishi ya sheria ya kuwaangamiza iliyokuwa imetolewa Shushani+ ili amwonyeshe Esta na kumweleza na kumwagiza+ kwamba aingie kwa mfalme na kumwomba kibali+ na kutoa ombi moja kwa moja mbele yake kwa ajili ya watu wake mwenyewe.+

9 Basi Hathaki+ akaingia na kumwambia Esta maneno ya Mordekai. 10 Ndipo Esta akamwambia Hathaki na kumwamuru hivi kumhusu Mordekai:+ 11 “Watumishi wote wa mfalme na watu wa wilaya za utawala wa mfalme wanajua kwamba mwanamume au mwanamke yeyote anayeingia kwa mfalme katika ua wa ndani+ bila kuitwa, mfalme ana sheria moja tu,+ kwamba mtu huyo auawe; ila tu mfalme akimnyooshea fimbo yake ya enzi ya dhahabu, ndipo atakapoendelea kuishi.+ Lakini mimi, kwa siku 30 sasa sijaitwa kuingia kwa mfalme.”

12 Nao wakamwambia Mordekai maneno ya Esta. 13 Ndipo Mordekai akasema Esta apewe jibu hili: “Usiwaze katika nafsi yako mwenyewe kwamba nyumba ya mfalme itaponyoka kuliko Wayahudi wengine wote.+ 14 Kwa maana ukinyamaza kabisa wakati huu, msaada na ukombozi wa Wayahudi utasimama kutoka mahali pengine;+ bali wewe pamoja na nyumba ya baba yako, mtaangamizwa. Na ni nani anayejua ikiwa si kwa ajili ya wakati kama huu kwamba umefikia heshima ya kifalme?”+

15 Basi Esta akasema Mordekai apewe jibu la kusema: 16 “Nenda, wakusanye Wayahudi wote waliopo Shushani+ na mfunge+ kwa ajili yangu, msile wala kunywa kwa siku tatu,+ usiku na mchana. Mimi pia pamoja na wanawake wangu vijana,+ nitafunga vivyo hivyo, na baada ya hapo nitaingia kwa mfalme, jambo ambalo ni kinyume cha sheria. Nami nikiangamia,+ na niangamie.” 17 Kwa hiyo Mordekai akaenda zake na kufanya kulingana na yote ambayo Esta alikuwa amemwamuru.

5 Na ikawa kwamba siku ya tatu+ Esta akavaa mavazi ya kifalme,+ kisha akasimama katika ua wa ndani+ wa nyumba ya mfalme kuelekeana na nyumba ya mfalme, mfalme akiwa ameketi katika kiti chake cha ufalme ndani ya nyumba ya kifalme kuelekeana na lango la nyumba. 2 Na ikawa kwamba, mara tu mfalme alipomwona Malkia Esta amesimama katika ua, akapata kibali+ machoni pake, naye mfalme akamnyooshea Esta fimbo yake ya enzi ya dhahabu+ iliyokuwa mkononi mwake. Basi Esta akakaribia na kuigusa ncha ya fimbo hiyo ya enzi.

3 Ndipo mfalme akamwambia: “Una nini, Ee Esta, malkia, na ombi lako ni nini?+ Hata nusu ya ufalme+—na upewe wewe!” 4 Naye Esta akasema: “Mfalme akiona vema, mfalme na aje leo pamoja na Hamani+ kwenye karamu+ ambayo nimemwandalia.” 5 Basi mfalme akasema: “Ninyi watu, mwambieni Hamani afanye haraka+ kulingana na neno la Esta.” Baadaye mfalme na Hamani wakaja kwenye karamu ambayo Esta alikuwa ameandaa.

6 Baada ya muda mfalme akamwambia Esta wakati wa karamu ya divai: “Ombi lako ni nini?+ Na upewe hilo! Hata nusu ya ufalme—na upewe wewe!” 7 Kwa hiyo Esta akajibu, akasema: “Haja yangu na ombi langu ni hili, 8 Ikiwa nimepata kibali machoni pa mfalme,+ na ikiwa inaonekana vema kwa mfalme kunipa haja yangu na kufanya kulingana na ombi langu, mfalme pamoja na Hamani na waje kwenye karamu ambayo nitawafanyia kesho, nami kesho nitafanya kulingana na neno la mfalme.”+

9 Basi Hamani akatoka siku hiyo akiwa na shangwe na furaha+ moyoni; lakini mara tu Hamani alipomwona Mordekai katika lango la mfalme+ na kwamba hakusimama+ wala kutetemeka kwa ajili yake,+ upesi Hamani akajawa na ghadhabu+ juu ya Mordekai. 10 Hata hivyo, Hamani akajizuia na kwenda nyumbani kwake. Kisha akatuma neno ili rafiki zake na Zereshi+ mke wake waletwe; 11 naye Hamani akawatangazia utukufu wa utajiri+ wake na hesabu kubwa ya wanawe+ na kila kitu ambacho mfalme alikuwa amemtukuza nacho na jinsi alivyokuwa amemwinua juu ya wakuu na watumishi wa mfalme.+

12 Tena Hamani akasema: “Zaidi ya hayo, Esta, malkia, hakumkaribisha mtu yeyote pamoja na mfalme kwenye karamu isipokuwa mimi,+ na kesho+ pia nimealikwa naye pamoja na mfalme. 13 Lakini hayo yote hayana faida yoyote kwangu ninapomwona yule Mordekai Myahudi ameketi katika lango la mfalme.” 14 Ndipo Zereshi mke wake na rafiki zake wote wakamwambia: “Na watengeneze mti+ wenye urefu wa mikono 50. Kisha asubuhi+ umwambie mfalme kwamba wamtundike Mordekai juu yake.+ Halafu uingie pamoja na mfalme kwenye karamu ukiwa na shangwe.” Basi jambo hilo likaonekana jema+ mbele ya Hamani, naye akautengeneza mti.+

6 Usiku huo usingizi wa mfalme ulimtoka.+ Kwa hiyo akasema kwamba kitabu cha kumbukumbu+ za mambo ya nyakati kiletwe. Kisha mambo hayo yakasomwa mbele ya mfalme. 2 Mwishowe wakapata maandishi ya habari ambazo Mordekai alikuwa ametoa+ juu ya Bigthana na Tereshi, maofisa wawili+ wa makao ya mfalme, watunza-milango, waliokuwa wametafuta kunyoosha mkono juu ya Mfalme Ahasuero. 3 Ndipo mfalme akasema: “Mordekai amefanyiwa heshima na jambo gani kubwa kwa ajili ya hayo?” Nao watumishi wa mfalme, wahudumu wake, wakasema: “Hajafanyiwa lolote.”+

4 Baadaye mfalme akasema: “Ni nani aliye katika ua?” Basi Hamani alikuwa amekuja katika ua wa nje+ wa nyumba ya mfalme ili kumwambia mfalme kwamba Mordekai atundikwe juu ya mti+ ambao alikuwa amemwekea tayari. 5 Nao watumishi wa mfalme wakamwambia: “Tazama, Hamani+ anasimama katika ua.” Kisha mfalme akasema: “Mwacheni aingie.”

6 Hamani alipoingia, mfalme akamwambia: “Mtu ambaye mfalme amependa kumheshimu afanyiwe nini?” Ndipo Hamani akasema moyoni mwake:+ “Mfalme angependa kumheshimu nani kuliko mimi?”+ 7 Kwa hiyo Hamani akamwambia mfalme: “Kuhusu mtu ambaye mfalme amependa kumheshimu, 8 na walete mavazi ya kifalme+ ambayo mfalme huvaa na farasi ambaye mfalme hupanda+ ambaye amevikwa taji la kifalme juu ya kichwa chake. 9 Na mmoja wa wakuu wenye cheo+ wa mfalme apewe yale mavazi na yule farasi; nao wamvike mtu ambaye mfalme amependa kumheshimu, nao wampandishe juu ya farasi katika kiwanja cha watu wote+ cha jiji,+ nao wapaaze sauti mbele yake, ‘Hivi ndivyo anavyofanyiwa mtu ambaye mfalme amependa kumheshimu.’”+ 10 Mara moja mfalme akamwambia Hamani: “Fanya haraka, chukua mavazi na farasi, kama ulivyosema, umfanyie hivyo Mordekai yule Myahudi anayeketi katika lango la mfalme. Usiache jambo lolote likose kutimia kati ya mambo yote uliyoyasema.”+

11 Ndipo Hamani akachukua mavazi+ na farasi, akamvika Mordekai+ na kumpandisha juu ya farasi kupitia katika kiwanja cha watu wote+ cha jiji na kupaaza sauti mbele yake:+ “Hivi ndivyo anavyofanyiwa mtu ambaye mfalme amependa kumheshimu.”+ 12 Baadaye Mordekai akarudi kwenye lango la mfalme.+ Lakini Hamani akafanya haraka kwenda nyumbani kwake akiomboleza, na kichwa chake kikiwa kimefunikwa.+ 13 Halafu Hamani akamsimulia Zereshi+ mke wake na rafiki zake wote juu ya mambo yote yaliyompata. Ndipo watu wake wenye hekima+ na Zereshi mke wake wakamwambia: “Ikiwa Mordekai, ambaye umeanza kuanguka mbele yake, anatoka katika uzao wa Wayahudi, wewe hutamshinda, bali bila shaka utaanguka mbele yake.”+

14 Walipokuwa bado wanasema naye, maofisa wa makao ya mfalme wakafika nao wakafanya haraka+ kumleta Hamani kwenye karamu+ ambayo Esta alikuwa ameandaa.

7 Ndipo mfalme na Hamani+ wakaingia ili kula karamu pamoja na Malkia Esta. 2 Basi mfalme akamwambia Esta siku ya pili pia wakati wa karamu ya divai:+ “Ombi lako ni nini,+ Ee Esta, malkia? Na upewe hilo.+ Na haja yako ni nini? Hata nusu ya ufalme+—na iwe hivyo!” 3 Kwa hiyo Esta, malkia, akajibu, akasema: “Ikiwa nimepata kibali machoni pako, Ee mfalme, na mfalme akiona vema, na nipewe nafsi+ yangu mwenyewe kuwa ombi langu na watu wangu+ kuwa haja yangu. 4 Kwa maana tumeuzwa,+ mimi na watu wangu, tuangamizwe, tuuawe na kuharibiwa.+ Basi ikiwa tungaliuzwa tuwe watumwa+ na wajakazi, ningalinyamaza kimya. Lakini taabu hii haifai ikiwa inamletea mfalme hasara.”

5 Sasa Mfalme Ahasuero akasema, ndiyo, akamwambia Malkia Esta: “Ni nani huyo,+ na yuko wapi mtu huyo ambaye amejipatia ujasiri+ wa kufanya hivyo?” 6 Ndipo Esta akasema: “Mtu huyo, mpinzani+ na adui,+ ni huyu Hamani mtu mbaya.”

Basi Hamani akaogopa sana+ kwa sababu ya mfalme na malkia. 7 Mfalme naye akasimama akiwa na ghadhabu+ akatoka kwenye karamu ya divai na kwenda katika bustani ya jumba la mfalme; Hamani naye akasimama kutoa ombi kwa Malkia Esta kwa ajili ya nafsi yake,+ maana aliona kuwa mfalme+ ameazimia mabaya+ juu yake. 8 Kisha mfalme akarudi kutoka katika bustani ya jumba la mfalme na kuingia katika nyumba ya karamu ya divai;+ naye Hamani alikuwa ameangukia kitanda+ alipokuwapo Esta. Basi mfalme akasema: “Je, malkia alalwe kinguvu vilevile, nami nimo nyumbani?” Neno hilo lilitoka kinywani mwa mfalme,+ nao wakaufunika uso wa Hamani. 9 Sasa Harbona,+ mmoja wa maofisa wa makao ya mfalme+ aliyetumikia mbele ya mfalme, akasema: “Pia, kuna mti+ wenye urefu wa mikono 50 ambao Hamani aliutengeneza kwa ajili ya Mordekai, aliyesema mema kumhusu mfalme,+ umesimama katika nyumba ya Hamani.” Basi mfalme akasema: “Mtundikeni juu yake.”+ 10 Nao wakamtundika Hamani juu ya mti+ ambao alikuwa ameweka tayari kwa ajili ya Mordekai;+ nayo ghadhabu ya mfalme ikapungua.

8 Siku hiyo Mfalme Ahasuero alimpa Esta, malkia, nyumba ya Hamani,+ ambaye aliwaonyesha Wayahudi uadui;+ naye Mordekai akaingia mbele ya mfalme, kwa maana Esta alikuwa amesema yeye ni nani kwake.+ 2 Kisha mfalme akavua pete yake ya muhuri+ aliyokuwa amempokonya Hamani, akampa Mordekai; naye Esta akamweka Mordekai juu ya nyumba ya Hamani.+

3 Tena, Esta akasema mara nyingine mbele ya mfalme na kuanguka chini miguuni pake, akalia na kumwomba+ kibali augeuzie mbali ubaya+ wa Hamani Mwagagi na hila+ yake aliyokuwa amepanga juu ya Wayahudi.+ 4 Ndipo mfalme akamnyooshea Esta fimbo ya enzi ya dhahabu,+ basi Esta akainuka na kusimama mbele ya mfalme. 5 Sasa akasema: “Ikiwa inaonekana vema kwa mfalme, na ikiwa nimepata kibali+ mbele yake na jambo hili linafaa mbele ya mfalme nami ni mwema machoni pake, na iandikwe kwamba zile barua zifutwe,+ ule mpango wa hila wa Hamani mwana wa Hamedatha Mwagagi,+ ambazo aliandika kuwaangamiza Wayahudi+ walio katika wilaya zote za utawala+ wa mfalme. 6 Kwa maana ninawezaje kuvumilia kutazama msiba utakaowapata watu wangu, nami ninawezaje kuvumilia kutazama maangamizi ya jamaa zangu?”

7 Basi Mfalme Ahasuero akamwambia Malkia Esta na Mordekai Myahudi: “Tazama! Nimempa Esta+ nyumba ya Hamani, naye wamemtundika mtini,+ kwa sababu alinyoosha mkono wake juu ya Wayahudi. 8 Nanyi andikeni kwa ajili ya Wayahudi kulingana na yaliyo mema machoni penu wenyewe katika jina la mfalme,+ nanyi myatie muhuri kwa pete ya mfalme; kwa maana maandishi ambayo yameandikwa kwa jina la mfalme na kutiwa muhuri kwa pete ya mfalme hayawezi kufutwa.”+

9 Basi waandishi+ wa mfalme wakaitwa wakati huo katika mwezi wa tatu, yaani, mwezi wa Sivani, siku ya 23 ya mwezi huo; na Wayahudi na maliwali+ na magavana na wakuu wa wilaya za utawala ambazo zilikuwa kutoka India mpaka Ethiopia, wilaya za utawala 127,+ wakaandikiwa kulingana na yote ambayo Mordekai aliamuru. Kila wilaya ya utawala kwa mtindo wao wa kuandika+ na kila kikundi cha watu kwa lugha+ yao, na Wayahudi kwa mtindo wao wa kuandika na kwa lugha+ yao.

10 Naye akaandika kwa jina la Mfalme+ Ahasuero na kutia muhuri+ kwa pete ya mfalme+ na kupeleka barua kwa mkono wa wajumbe waliopanda farasi+ wenye kusafirisha barua wanaotumiwa katika utumishi wa kifalme, wana-farasi wenye mbio, 11 kwamba mfalme alitoa ruhusa kwa Wayahudi walio katika majiji yote mbalimbali wajikusanye+ na kusimama kwa ajili ya nafsi zao, waangamize, waue, na kuharibu jeshi lote la watu+ na wilaya za utawala zilizokuwa zikiwaonyesha uadui, watoto kwa wanawake, na kupora nyara zao,+ 12 siku moja+ katika wilaya zote za utawala za Mfalme Ahasuero, siku ya kumi na tatu+ ya mwezi wa kumi na mbili, yaani, mwezi wa Adari.+ 13 Nakala+ ya maandishi hayo ingetolewa kama sheria katika wilaya zote mbalimbali za utawala, ikitangaza kwa vikundi vyote vya watu, kwamba Wayahudi walipaswa kuwa tayari kwa ajili ya siku hiyo ili wajilipizie kisasi+ juu ya adui zao. 14 Wajumbe+ nao, wakiwa wamepanda farasi wenye kusafirisha barua wanaotumiwa katika utumishi wa kifalme, wakaondoka, wakiwa wanachochewa kwenda mbele na kuendeshwa mbio+ kwa sababu ya neno la mfalme; na sheria hiyo ilitolewa katika ngome ya Shushani.+

15 Naye Mordekai akatoka mbele ya mfalme akiwa amevaa mavazi ya kifalme+ ya bluu na kitani, taji kubwa la dhahabu, na kanzu ya kitambaa laini,+ ya sufu iliyotiwa rangi ya zambarau.+ Na jiji la Shushani likapaaza sauti na kushangilia.+ 16 Kwa Wayahudi kukawa nuru na kushangilia+ na furaha na heshima. 17 Na katika wilaya zote mbalimbali za utawala na katika majiji yote mbalimbali ambako neno la mfalme na sheria yake ilifika kulikuwa na shangwe na furaha kwa Wayahudi, karamu+ na siku njema; na watu wengi+ wa nchi wakawa wanajitangaza wenyewe kuwa Wayahudi,+ maana hofu+ ya Wayahudi ilikuwa imewashika.

9 Na katika mwezi wa kumi na mbili, yaani, mwezi wa Adari,+ siku ya kumi na tatu ya mwezi huo, wakati ulipofika wa kutimiza neno la mfalme na sheria yake,+ siku ambayo adui za Wayahudi walikuwa wamengojea kuwatawala, mambo yaligeuka yakawa kinyume, kwa maana Wayahudi waliwatawala wale waliowachukia.+ 2 Wayahudi walijikusanya+ katika majiji yao katika wilaya zote za utawala wa Mfalme Ahasuero+ ili kunyoosha mikono yao juu ya wale waliotafuta kuwaumiza,+ wala hakuna hata mtu mmoja aliyeweza kusimama mbele yao, kwa maana vikundi vyote vya watu walikuwa wameshikwa na hofu+ kwa sababu yao. 3 Na wakuu wote+ wa wilaya za utawala na maliwali+ na magavana na watendaji wa kazi+ za mfalme walikuwa wakiwasaidia Wayahudi, kwa maana walikuwa wameshikwa na hofu+ kwa sababu ya Mordekai. 4 Kwa maana Mordekai alikuwa mkuu+ katika nyumba ya mfalme na sifa yake+ ilivuma kotekote katika wilaya zote za utawala, kwa sababu huyo Mordekai alikuwa akizidi kuwa mkuu.+

5 Nao Wayahudi wakawapiga adui zao wote kwa mauaji ya upanga,+ wakawaua na kuwaangamiza, nao wakawatendea walivyotaka wale waliowachukia.+ 6 Na katika ngome ya Shushani+ Wayahudi waliwaua na kuwaangamiza watu mia tano. 7 Pia, Parshandatha na Dalfoni na Aspatha 8 na Poratha na Adalia na Aridatha 9 na Parmashta na Arisai na Aridai na Vaizatha, 10 wana kumi+ wa Hamani+ mwana wa Hamedatha, yule aliyewaonyesha Wayahudi uadui,+ wakawaua hao; lakini hawakunyoosha mkono wao juu ya nyara.+

11 Siku hiyo hesabu ya waliouawa katika ngome ya Shushani ikaletwa mbele ya mfalme.

12 Na mfalme akamwambia Malkia Esta:+ “Katika ngome+ ya Shushani Wayahudi wamewaua na kuwaangamiza watu mia tano pamoja na wana kumi wa Hamani. Katika wilaya nyinginezo za utawala+ wa mfalme wamefanya nini?+ Na ombi lako ni nini? Na upewe hilo.+ Na haja yako zaidi ni nini?+ Na ifanywe.” 13 Kwa hiyo Esta akasema: “Ikiwa kwa mfalme inaonekana vema,+ Wayahudi walio katika Shushani na wapewe ruhusa kesho pia kufanya kulingana na sheria ya leo;+ na hao wana kumi wa Hamani watundikwe juu ya mti.”+ 14 Basi mfalme akasema ifanywe hivyo.+ Ndipo sheria ikatolewa katika Shushani, na wale wana kumi wa Hamani wakatundikwa mtini.

15 Na Wayahudi waliokuwa Shushani wakajikusanya pia siku ya kumi na nne+ ya mwezi wa Adari, nao wakawaua watu mia tatu Shushani; lakini hawakunyoosha mkono wao juu ya nyara.+

16 Na wale Wayahudi wengine waliokuwa katika wilaya za utawala+ wa mfalme, walijikusanya, wakasimama kwa ajili ya nafsi+ zao, wakajilipizia kisasi+ juu ya adui zao na kuua watu 75,000 kati ya wale waliowachukia; lakini hawakunyoosha mkono wao juu ya nyara, 17 katika siku ya kumi na tatu ya mwezi wa Adari; na kukawa na pumziko siku ya kumi na nne ya mwezi huo, nayo ikafanywa kuwa siku ya karamu+ na kushangilia.+

18 Nao Wayahudi waliokuwa Shushani, wakajikusanya siku ya kumi na tatu+ na siku ya kumi na nne ya mwezi huo, kukawa na pumziko siku ya kumi na tano ya mwezi huo, nayo ikafanywa kuwa siku ya karamu na kushangilia.+ 19 Ndiyo sababu Wayahudi wa mashambani, waliokaa katika majiji ya wilaya za utawala zilizo kandokando, walikuwa wakiifanya siku ya kumi na nne ya mwezi wa Adari+ kuwa siku ya kushangilia,+ ya karamu na siku njema+ na ya kupelekeana mafungu+ ya vitu.

20 Naye Mordekai+ akaandika mambo hayo na kuagiza barua zipelekwe kwa Wayahudi wote waliokuwa katika wilaya zote za utawala+ wa Mfalme Ahasuero, zilizo karibu na zilizo mbali pia, 21 kuwawekea wajibu+ wawe wakishika kwa ukawaida siku ya kumi na nne ya mwezi wa Adari na siku ya kumi na tano ya mwezi huo mwaka baada ya mwaka, 22 kulingana na siku ambazo Wayahudi walipumzika kutokana na adui+ zao na mwezi ambao huzuni yao iligeuzwa kuwa shangwe na maombolezo+ yakawa siku njema, wazishike ziwe siku za karamu na kushangilia na kupelekeana mafungu+ ya vitu na zawadi kwa maskini.+

23 Nao Wayahudi wakakubali mambo ambayo walikuwa wameanza kufanya na yale ambayo Mordekai alikuwa amewaandikia. 24 Kwa maana Hamani+ mwana wa Hamedatha+ Mwagagi,+ yule aliyewaonyesha Wayahudi wote uadui,+ alikuwa amepanga hila juu ya Wayahudi ili kuwaangamiza,+ naye alikuwa amefanya Puri,+ yaani, Kura,+ ipigwe, ili kuwahangaisha na kuwaangamiza. 25 Lakini mfalme alisema kwa barua wakati Esta alipoingia mbele yake:+ “Hila+ mbaya ambayo amepanga juu ya Wayahudi na irudi juu ya kichwa chake mwenyewe”;+ nao wakamtundika pamoja na wanawe juu ya mti.+ 26 Ndiyo sababu waliziita siku hizo Purimu, kufuatia jina la Puri.+ Ndiyo sababu, kulingana na maneno yote ya barua hii+ na yote ambayo walikuwa wameona kuhusiana na hayo na yale ambayo yalikuwa yamewafikia, 27 Wayahudi, uzao wao, na wale wote waliojiunga nao,+ walijiwekea wajibu na kukubali kwamba usipitilie mbali wajibu wa kuzishika kwa ukawaida siku hizo mbili kulingana na mambo yaliyoandikwa kuwahusu na kulingana na wakati wake uliowekwa mwaka baada ya mwaka. 28 Na siku hizo zilipasa kukumbukwa na kushikwa na kizazi baada ya kizazi, kila familia, kila wilaya ya utawala na kila jiji, na siku hizo za Purimu zisipitilie mbali kutoka katikati ya Wayahudi wala ukumbusho+ wake usikome kati ya uzao wao.

29 Na Malkia Esta, binti ya Abihaili,+ na Mordekai Myahudi, wakaandika kwa mamlaka yote ili kuthibitisha barua hii ya pili iliyohusu Purimu. 30 Kisha akatuma barua kwa Wayahudi wote katika zile wilaya 127, za utawala+ wa Ahasuero,+ katika maneno ya amani na kweli,+ 31 ili kuthibitisha siku hizo za Purimu kwa wakati wake uliowekwa, kama vile Mordekai Myahudi, na Malkia Esta walivyokuwa wamewawekea kuwa wajibu,+ na kama vile walivyokuwa wamejiwekea kuwa wajibu juu ya nafsi zao wenyewe na juu ya uzao wao,+ mambo ya kufunga+ na kilio chao cha kuomba msaada.+ 32 Na neno la Esta likathibitisha mambo hayo ya Purimu,+ nayo yakaandikwa katika kitabu.

10 Naye Mfalme Ahasuero akaweka kazi ya kulazimishwa+ juu ya nchi na visiwa+ vya bahari.

2 Basi kuhusu kazi zake zote zenye nguvu na uwezo wake na taarifa kamili ya ukuu wa Mordekai+ ambao mfalme alimtukuza+ nao, je, mambo hayo hayakuandikwa katika Kitabu cha mambo+ ya nyakati ya wafalme wa Umedi na Uajemi?+ 3 Kwa maana Mordekai Myahudi alikuwa wa pili+ kwa Mfalme Ahasuero naye alikuwa mkuu kati ya Wayahudi na alikubaliwa na wengi wa ndugu zake, akifanya kazi kwa ajili ya mema ya watu wake na kusema amani+ kwa uzao wao wote.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki