Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • bi12 2 Wakorintho 1:1-13:14
  • Barua ya Pili kwa Wakorintho

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Barua ya Pili kwa Wakorintho
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Barua ya Pili kwa Wakorintho

Barua ya Pili kwa Wakorintho

1 Paulo, mtume+ wa Kristo Yesu kupitia mapenzi ya Mungu, na Timotheo+ ndugu yetu kwa kutaniko la Mungu lililo katika Korintho, pamoja na watakatifu+ wote walio katika Akaya+ yote:

2 Na muwe na fadhili zisizostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo.+

3 Abarikiwe Mungu na Baba+ ya Bwana wetu Yesu Kristo, Baba ya rehema+ nyororo na Mungu wa faraja+ yote, 4  ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote,+ ili tuweze kuwafariji+ wale walio katika namna yoyote ya dhiki kupitia faraja ambayo sisi wenyewe tunafarijiwa na Mungu.+ 5 Kwa maana kama vile mateso kwa ajili ya Kristo yalivyo mengi katika sisi,+ vivyo hivyo faraja tunayopata pia ni nyingi kupitia Kristo.+ 6 Basi kama tumo katika dhiki, hiyo ni kwa ajili ya faraja na wokovu+ wenu; au kama tunafarijiwa, hiyo ni kwa ajili ya faraja yenu inayotenda ili kuwafanya mvumilie mateso yaleyale ambayo sisi pia tunateseka.+ 7 Na kwa hiyo tumaini letu kwa ajili yenu haliyumbi-yumbi, tukijua kama tunavyojua kwamba, kama vile mlivyo washiriki wa hayo mateso, vivyo hivyo ninyi pia mtaishiriki faraja.+

8 Kwa maana sisi hatutaki ninyi mkose kujua, akina ndugu, juu ya dhiki iliyotupata katika wilaya ya Asia,+ kwamba tulikuwa chini ya mkazo mkubwa mno unaoshinda nguvu zetu, hivi kwamba hatukuwa na uhakika kabisa hata juu ya uhai wetu.+ 9 Kwa kweli, tuliona ndani yetu wenyewe kwamba tumepokea hukumu ya kifo. Ilikuwa hivyo ili uhakika+ wetu uwe, si katika sisi wenyewe, bali katika Mungu ambaye huwafufua wafu.+ 10 Kutoka katika kitu kikubwa sana kama kifo alituokoa naye atatuokoa;+ na tumaini letu limo katika yeye kwamba atatuokoa zaidi pia.+ 11 Ninyi pia mnaweza kushiriki kusaidia kwa dua yenu kwa ajili yetu,+ ili wengi watoe shukrani+ kwa ajili yetu kwa lile ambalo tumepewa kwa fadhili kutokana na sala za watu wengi.+

12 Kwa maana jambo tunalojisifia ni hili, ambalo dhamiri yetu inalitolea ushahidi,+ kwamba kwa utakatifu na unyoofu wa moyo wa kimungu, si kwa hekima ya kimwili+ bali kwa fadhili zisizostahiliwa za Mungu, tumejiendesha katika ulimwengu, lakini hasa kuwaelekea ninyi. 13 Kwa maana kwa kweli hatuwaandikii ninyi mambo isipokuwa yale mnayoyajua vema au kuyatambua pia; na ambayo mimi natumaini mtaendelea kuyatambua mpaka mwisho,+ 14 kama vile ambavyo mmetambua pia, kwa kadiri fulani, kwamba sisi ni sababu yenu ya kujisifu,+ kama vile ninyi mtakavyokuwa kwetu pia katika siku ya Bwana wetu Yesu.+

15 Kwa hiyo, nikiwa na uhakika huu, nilikuwa nikikusudia hapo mbeleni kuja kwenu,+ ili muwe na pindi ya pili+ ya kuwa na shangwe, 16 nami niende Makedonia+ baada ya kukaa kidogo kwenu, na kurudi kutoka Makedonia kuja kwenu+ nanyi mnisindikize+ kwenda Yudea. 17 Basi, nilipokuwa nikikusudia hivyo, je, nilifanya mambo kijuujuu?+ Au mambo yale ninayokusudia, je, mimi nayakusudia kulingana na mwili,+ ili kwamba niseme “Ndiyo, Ndiyo” na “Siyo, Siyo”?+ 18 Lakini Mungu anaweza kutegemewa ili neno letu kwenu lisiwe ni Ndiyo na pia Siyo. 19 Kwa maana Mwana wa Mungu,+ Kristo Yesu, aliyehubiriwa katikati yenu kupitia sisi, yaani, kupitia mimi na Silvano na Timotheo,+ hakuwa Ndiyo na pia Siyo, bali Ndiyo imekuwa Ndiyo kuhusiana naye.+ 20 Kwa maana hata ahadi+ za Mungu ziwe nyingi kadiri gani, zimekuwa Ndiyo kwa njia yake.+ Kwa hiyo kupitia yeye pia “Amina”+ husemwa kwa Mungu kwa ajili ya utukufu kupitia sisi. 21 Lakini yeye ambaye hutoa uhakikisho kwamba ninyi na sisi ni wa Kristo na yeye ambaye ametutia mafuta+ ni Mungu. 22 Yeye pia ametia muhuri+ wake juu yetu naye ametupa sisi rehani+ ya kitakachokuja, yaani, roho,+ katika mioyo yetu.

23 Sasa namwita Mungu awe shahidi+ juu ya nafsi yangu mwenyewe ya kuwa ni kwa kuwahurumia ninyi+ kwamba bado sijaja Korintho. 24 Si kwamba sisi ndio mabwana+ juu ya imani yenu, bali sisi ni wafanyakazi wenzi+ kwa shangwe yenu, kwa maana ni kwa imani+ yenu kwamba ninyi mnasimama.+

2 Kwa maana hili ndilo nimejiamulia mwenyewe, nisije kwenu tena kwa huzuni.+ 2 Kwa maana nikiwahuzunisha ninyi,+ kwa kweli ni nani aliyeko wa kunichangamsha isipokuwa yeye ambaye mimi ninamhuzunisha? 3 Na kwa hiyo niliandika jambo hili, ili, nitakapokuja, nisihuzunike+ kwa sababu ya wale ambao ninapaswa kushangilia juu yao;+ kwa sababu nina uhakika+ katika ninyi nyote kwamba shangwe niliyo nayo ni ile yenu nyote. 4 Kwa maana kutokana na dhiki nyingi na maumivu makali ya moyo niliwaandikia ninyi kwa machozi mengi,+ si ili mhuzunishwe,+ bali ili muujue upendo nilio nao hasa zaidi kwa ajili yenu.

5 Basi ikiwa yeyote amesababisha huzuni,+ amehuzunisha, si mimi, bali ninyi nyote kwa kadiri fulani—nisiwe mkali mno kwa yale ninayosema. 6 Kemeo+ hili linalotolewa na walio wengi linamtosha mtu wa namna hiyo, 7 ili kwamba, kinyume chake sasa, mnapaswa kumsamehe+ kwa fadhili na kumfariji, ili kwa njia fulani mtu huyo asimezwe na huzuni yake ya kupita kiasi.+ 8 Kwa hiyo nawahimiza ninyi kumthibitishia upendo+ wenu. 9 Kwa maana kwa lengo hili pia ninaandika ili kuhakikisha uthibitisho wenu, kama ninyi ni watiifu katika mambo yote.+ 10 Jambo lolote ambalo mnamsamehe yeyote kwa fadhili, mimi vilevile namsamehe.+ Kwa kweli, kwa habari yangu mimi, lolote lile ambalo nimesamehe kwa fadhili, ikiwa nimesamehe kwa fadhili jambo lolote, imekuwa ni kwa ajili yenu machoni pa Kristo; 11 ili Shetani+ asitushinde akili, kwa maana sisi hatukosi kuzijua mbinu zake.+

12 Basi nilipofika Troa+ kutangaza habari njema juu ya Kristo, nami nikafunguliwa mlango katika Bwana,+ 13 sikupata kitulizo katika roho yangu kwa sababu ya kukosa kumkuta Tito+ ndugu yangu, bali niliwaaga kisha nikaondoka kwenda Makedonia.+

14 Lakini Mungu apewe shukrani, ambaye sikuzote hutuongoza+ katika maandamano yenye shangwe ya ushindi kwa kushirikiana+ na Kristo naye huifanya harufu ya ujuzi juu yake yeye ifahamike kupitia sisi kila mahali!+ 15 Kwa maana kwa Mungu sisi ni harufu tamu+ ya Kristo katikati ya wale wanaookolewa na katikati ya wale wanaoangamia;+ 16 kwa hawa wa mwisho ni harufu inayotoka katika kifo mpaka kifo,+ kwa wale wa kwanza ni harufu inayotoka katika uzima mpaka uzima. Na ni nani ambaye ana sifa za kustahili vya kutosha kwa ajili ya mambo haya?+ 17 Ni sisi; kwa maana sisi si wachuuzi wa neno la Mungu+ kama watu wengi walivyo,+ bali tunasema kwa unyoofu wa moyo, ndiyo, tukiwa waliotumwa kutoka kwa Mungu, machoni pa Mungu, kwa kushirikiana na Kristo.+

3 Je, tunaanza tena kujipendekeza wenyewe?+ Au je, sisi, labda, kama watu fulani, tunahitaji barua+ za pendekezo kuja au kutoka kwenu? 2 Ninyi wenyewe ndio barua yetu,+ iliyoandikwa juu ya mioyo yetu na kujulikana na kusomwa na wanadamu wote.+ 3 Kwa maana ninyi mnaonyeshwa kuwa barua ya Kristo ambayo sisi tuliandika tukiwa wahudumu,+ iliyoandikwa si kwa wino bali kwa roho+ ya Mungu aliye hai, si juu ya mabamba ya mawe,+ bali juu ya mabamba ya nyama, juu ya mioyo.+

4 Basi kupitia Kristo tuna uhakika+ wa namna hii kwa Mungu. 5 Si kwamba sisi wenyewe tuna sifa za kustahili vya kutosha kuhesabu kuwa jambo lolote linatoka kwetu wenyewe,+ bali kuwa kwetu na sifa za kustahili vya kutosha hutoka kwa Mungu,+ 6 ambaye kwa kweli ametustahilisha vya kutosha kuwa wahudumu wa agano jipya,+ si wa sheria zilizoandikwa,+ bali wa roho;+ kwa maana sheria zilizoandikwa huleta hukumu+ ya kifo, bali roho hufanya kuwa hai.+

7 Zaidi ya hayo, ikiwa sheria ambazo hutoa kifo+ na ambazo zilichongwa kwa herufi katika mawe+ zilikuja kwa utukufu,+ hivi kwamba wana wa Israeli hawakuweza kuutazama uso wa Musa kwa sababu ya utukufu wa uso wake,+ utukufu ambao ungekuja kuondolewa mbali, 8 kwa nini kutolewa kwa roho+ kusiwe kwenye utukufu zaidi?+ 9 Kwa maana ikiwa sheria zilizotoa hukumu ya hatia+ zilikuwa zenye utukufu,+ basi kutolewa kwa uadilifu+ kunakuwa kwenye utukufu mwingi zaidi.+ 10 Kwa kweli, hata kile ambacho wakati mmoja kilifanywa kuwa na utukufu kimevuliwa utukufu kwa habari hii,+ kwa sababu ya utukufu unachokizidi ubora.+ 11 Kwa maana ikiwa kile ambacho kingeondolewa mbali kiliingizwa na utukufu,+ basi kile ambacho kinabaki kingekuwa na utukufu hata zaidi.+

12 Kwa hiyo, kwa kuwa tuna tumaini la namna hiyo,+ tunatumia uhuru mkubwa wa kusema, 13 nasi hatufanyi kama Musa alipokuwa akiweka utaji+ juu ya uso wake, ili wana wa Israeli wasitazame mwisho+ wa kile ambacho kingeondolewa mbali. 14 Lakini nguvu zao za akili zilitiwa uzito.+ Kwa maana mpaka leo, utaji uleule unadumu bila kuondolewa wakati wa usomaji wa agano la zamani,+ kwa sababu unaondolewa mbali kwa njia ya Kristo.+ 15 Kwa kweli, mpaka leo wakati wowote maandishi ya Musa yanaposomwa,+ utaji hukaa juu ya mioyo yao.+ 16 Lakini kunapokuwa na tendo la kugeuka kumwelekea Yehova, utaji huondolewa mbali.+ 17 Basi Yehova ndiye Roho;+ na mahali palipo na roho+ ya Yehova,+ pana uhuru.+ 18 Na sisi sote,+ wakati tunapotoa kama vioo mrudisho wa utukufu wa Yehova+ tukiwa na nyuso zisizo na utaji, tunageuzwa+ na kuwa katika mfano+ uleule kutoka utukufu mpaka utukufu,+ sawasawa kabisa na anavyofanya Yehova+ aliye Roho.

4 Hiyo ndiyo sababu, kwa kuwa sisi tuna huduma+ hii kulingana na rehema tuliyoonyeshwa,+ hatufi moyo; 2 bali tumeyakataa mambo ya kichinichini ambayo ni ya kuonea aibu,+ si kutembea kwa ujanja, wala kulichanganya na kitu neno la Mungu,+ bali kwa kufanya kweli iwe wazi tukijipendekeza kwa kila dhamiri ya kibinadamu machoni pa Mungu.+ 3 Basi, ikiwa kwa kweli habari njema tunayotangaza imefunikwa utaji, imefunikwa utaji katikati ya wale wanaoangamia,+ 4 ambao katikati yao mungu wa mfumo huu wa mambo+ amezipofusha akili za wasioamini,+ ili nuru+ ya habari njema yenye utukufu+ juu ya Kristo, aliye mfano+ wa Mungu, isipenyeze mwangaza.+ 5 Kwa maana sisi tunahubiri, si juu yetu wenyewe, bali juu ya Kristo Yesu kuwa ni Bwana,+ na sisi wenyewe kuwa ni watumwa+ wenu kwa ajili ya Yesu. 6 Kwa maana Mungu ndiye aliyesema: “Nuru na iangaze kutoka katika giza,”+ naye ameangaza juu ya mioyo yetu ili kuimulika+ kwa ujuzi+ wenye utukufu juu ya Mungu kwa uso wa Kristo.+

7 Hata hivyo, sisi tuna hazina+ hii katika vyombo+ vya udongo,+ ili nguvu+ zinazopita zile za kawaida ziwe za Mungu+ na si zile za kutoka ndani yetu wenyewe.+ 8 Tunakazwa katika kila njia,+ lakini hatubanwi kupita kiasi cha kuweza kusonga; tunafadhaishwa, lakini si bila njia ya kutokea kabisa;+ 9 tunateswa, lakini hatuachwi kabisa bila msaada;+ tunaangushwa chini,+ lakini hatuangamizwi.+ 10 Sikuzote kila mahali katika mwili wetu tunavumilia matendo yenye kuleta kifo ambayo Yesu alitendewa,+ ili uzima wa Yesu ufunuliwe pia katika mwili wetu.+ 11 Kwa maana sisi tunaoishi tunaletwa uso kwa uso na kifo+ sikuzote kwa ajili ya Yesu, ili uzima wa Yesu ufunuliwe pia katika mwili wetu unaoweza kufa.+ 12 Kwa sababu hiyo kifo kinafanya kazi ndani yetu, lakini uzima ndani yenu.+

13 Basi kwa sababu tuna roho ileile ya imani kama ile ambayo imeandikwa hivi juu yake: “Mimi nilionyesha imani, kwa hiyo nikasema,”+ sisi pia tunaonyesha imani na kwa hiyo tunasema, 14 tukijua kwamba yeye ambaye alimfufua Yesu atatufufua sisi pia pamoja na Yesu naye atatutokeza sisi pamoja nanyi.+ 15 Kwa maana mambo yote ni kwa ajili yenu,+ ili fadhili zisizostahiliwa zilizozidishwa ziwe nyingi kwa sababu ya kutoa shukrani kwa wengi zaidi kwa utukufu wa Mungu.+

16 Kwa hiyo hatufi moyo, lakini hata ikiwa mtu tuliye kwa nje anachakaa, hakika mtu tuliye kwa ndani+ anafanywa upya siku baada ya siku. 17 Kwa maana ingawa dhiki ni ya dakika na ni nyepesi,+ hiyo inatufanyizia utukufu wenye uzito mkubwa zaidi na zaidi na ni wa milele;+ 18 huku tukiendelea kukaza macho yetu, si juu ya vitu vinavyoonekana, bali juu ya vitu visivyoonekana.+ Kwa maana vitu vinavyoonekana ni vya muda,+ lakini vitu visivyoonekana ni vya milele.+

5 Kwa maana tunajua kwamba nyumba yetu ya kidunia,+ hema+ hili, ikivunjwa,+ tutapata jengo kutoka kwa Mungu, nyumba isiyojengwa kwa mikono,+ ya milele+ mbinguni. 2 Kwa maana tunaugua+ kwelikweli katika nyumba hii ya kukaa, tukitamani kwa bidii kuvaa ile yetu kutoka mbinguni,+ 3 ili kwamba, tukiisha kuivaa kwelikweli, hatutapatikana tukiwa uchi.+ 4 Kwa kweli, sisi tulio katika hema hili tunaugua, tukilemewa; kwa sababu tunataka, si kulivua, bali kuvaa lile lingine,+ ili uhai ukimeze kile kinachoweza kufa.+ 5 Basi yeye aliyetutokeza kwa ajili ya jambo hili ni Mungu,+ aliyetupa sisi rehani+ ya kitakachokuja, yaani, roho.+

6 Kwa hiyo sikuzote sisi tuna uhodari mwingi na tunajua kwamba, tukiwa tungali na makao yetu katika mwili, hatupo mahali alipo Bwana,+ 7 kwa maana tunatembea kwa imani, si kwa kuona.+ 8 Lakini sisi tuna uhodari mwingi na tunapendezwa vema tusiwepo katika mwili na badala yake tufanye makao yetu pamoja na Bwana.+ 9 Kwa hiyo pia tunaifanya iwe shabaha yetu kwamba, kama tuna makao yetu pamoja naye au tukiwa hatupo pamoja naye,+ tuweze kukubalika kwake.+ 10 Kwa maana sisi sote lazima tufunuliwe mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo,+ ili kila mmoja apate thawabu yake kwa ajili ya mambo yaliyofanywa kupitia mwili, kulingana na mambo ambayo ametenda, kama ni mema au ni maovu.+

11 Kwa hiyo, kwa kuwa tunajua kumwogopa+ Bwana, tunaendelea kuwashawishi+ watu, lakini sisi tumefunuliwa kwa Mungu. Hata hivyo, natumaini kwamba tumefunuliwa pia kwa dhamiri+ zenu. 12 Hatujipendekezi+ wenyewe tena kwenu, bali tunawapa ninyi kichocheo cha kujisifu kuhusiana na sisi,+ ili mpate kuwa na jibu la kuwapa wale ambao hujisifu juu ya sura ya nje+ lakini si juu ya moyo.+ 13 Kwa maana ikiwa tulikuwa tumerukwa na akili+ yetu, ilikuwa ni kwa ajili ya Mungu; ikiwa tuna utimamu wa akili,+ ni kwa ajili yenu. 14 Kwa maana upendo alio nao Kristo hutulazimisha, kwa sababu hili ndilo tumehukumu, kwamba mtu mmoja alikufa kwa ajili ya wote;+ kwa hiyo, basi, wote walikuwa wamekufa; 15 naye alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe,+ bali kwa ajili ya yeye+ aliyekufa kwa ajili yao na kufufuliwa.+

16 Kwa hiyo tangu sasa na kuendelea sisi hatumjui mtu yeyote kulingana na mwili.+ Hata kama tumemjua Kristo kulingana na mwili,+ hakika sasa hatumjui hivyo tena.+ 17 Basi ikiwa yeyote yuko katika muungano na Kristo, yeye ni kiumbe kipya;+ mambo ya zamani yalipitilia mbali,+ tazama! mambo mapya yamekuja kuwako.+ 18 Lakini mambo yote yametoka kwa Mungu, aliyetupatanisha+ sisi kwake mwenyewe kupitia Kristo na kutupa sisi huduma+ ya upatanisho, 19 yaani, kwamba Mungu kupitia Kristo+ alikuwa akiupatanisha ulimwengu+ kwake mwenyewe,+ bila kuwahesabia makosa+ yao, naye alitukabidhi sisi lile neno+ la upatanisho.+

20 Kwa hiyo sisi+ ni mabalozi+ walio badala ya Kristo,+ kana kwamba Mungu alikuwa akisihi kupitia sisi.+ Kama walio badala ya Kristo tunaomba:+ “Mpatanishwe pamoja na Mungu.” 21 Yeye ambaye hakujua dhambi+ alimfanya kuwa dhambi+ kwa ajili yetu, ili sisi tuwe uadilifu wa Mungu+ kupitia yeye.

6 Huku tukifanya kazi pamoja naye,+ tunawasihi ninyi pia msipokee fadhili zisizostahiliwa za Mungu kisha mkose kusudi lake.+ 2 Kwa maana anasema: “Katika wakati unaokubalika nilikusikia, na katika siku ya wokovu nilikusaidia.”+ Tazama! Sasa ndio wakati unaokubalika+ hasa. Tazama! Sasa ndiyo siku ya wokovu.+

3 Sisi hatutoi sababu yoyote ya kukwaza+ kwa njia yoyote, ili huduma yetu isilaumiwe;+ 4 bali katika kila njia tunajipendekeza+ kuwa wahudumu wa Mungu, kwa kuvumilia mengi, kwa dhiki, kwa hali za uhitaji, kwa magumu,+ 5 kwa mapigo, kwa vifungo vya gerezani,+ kwa machafuko, kwa kazi za jasho, kwa kukosa usingizi usiku, kwa nyakati za kuwa bila chakula,+ 6 kwa utakato, kwa ujuzi, kwa ustahimilivu,+ kwa fadhili,+ kwa roho takatifu, kwa upendo usio na unafiki,+ 7 kwa kusema maneno ya kweli, kwa nguvu za Mungu;+ kupitia silaha+ za uadilifu upande wa mkono wa kuume na wa kushoto, 8 kupitia utukufu na aibu, kupitia habari ambazo ni mbaya na habari ambazo ni njema; kama wanaodanganya+ na bado ni wenye kusema kweli, 9 kama wasiojulikana na bado ni wenye kutambuliwa,+ kama wanaokufa na bado, tazama! tunaishi,+ kama wanaotiwa nidhamu+ na bado hatukabidhiwi kwenye kifo,+ 10 kama walio na huzuni lakini wenye kushangilia sikuzote, kama maskini lakini wenye kuwatajirisha wengi, kama wasio na kitu chochote na bado wenye kuwa na vitu vyote.+

11 Kinywa chetu kimefunguliwa kwenu, enyi Wakorintho, moyo+ wetu umepanuka. 12 Ninyi hamjasongwa mkakosa nafasi ndani yetu,+ lakini mmesongwa mkakosa nafasi katika upendo wenu mwororo.+ 13 Kwa hiyo, yakiwa kama malipo—mimi nasema kana kwamba ni kwa watoto+—ninyi, pia, panukeni.

14 Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.+ Kwa maana kuna ushirika gani kati ya uadilifu na uasi-sheria?+ Au nuru ina ushirika gani na giza?+ 15 Na zaidi, kuna upatano gani kati ya Kristo na Beliali?+ Au mtu mwaminifu ana fungu+ gani na asiye mwamini? 16 Na hekalu la Mungu lina upatano gani na sanamu?+ Kwa maana sisi ni hekalu+ la Mungu aliye hai; kama Mungu alivyosema: “Mimi nitakaa katikati yao+ na kutembea katikati yao, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.”+ 17 “ ‘Kwa hiyo tokeni katikati yao, na mjitenge,’ asema Yehova, ‘na mwache kugusa kitu kilicho najisi’ ”;+ “ ‘nami nitawakaribisha ndani.’ ”+ 18 “ ‘Nami nitakuwa baba kwenu,+ nanyi mtakuwa wana na mabinti kwangu,’+ asema Yehova Mweza-Yote.”+

7 Kwa hiyo, wapendwa, kwa kuwa tuna ahadi hizi,+ acheni tujisafishe+ wenyewe kila unajisi wa mwili na roho,+ tukiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.+

2 Mtupe sisi nafasi.+ Hatujamkosea yeyote, hatujamharibu yeyote, hatujamtumia yeyote kwa kujifaidi.+ 3 Sisemi jambo hili ili niwahukumu ninyi. Kwa maana tayari nimesema kwamba ninyi mko ndani ya mioyo yetu ili kufa na kuishi pamoja nasi.+ 4 Mimi nina uhuru mkubwa wa kusema kuwaelekea ninyi. Ninajisifu kwa njia kubwa kuhusiana nanyi.+ Nimejawa na faraja,+ ninafurika kwa shangwe katika taabu yetu yote.+

5 Kwa kweli, tulipofika Makedonia,+ mwili wetu haukupata kitulizo,+ bali tuliendelea kutaabishwa+ katika kila namna—kulikuwa na mapigano nje, woga ndani. 6 Hata hivyo Mungu, ambaye huwafariji+ wale walioshushwa chini, alitufariji kwa kuwapo kwa Tito; 7 lakini si kwa kuwapo kwake tu, bali pia kwa faraja ambayo alikuwa amefarijiwa juu yenu, kwa kuwa alituletea habari+ tena juu ya tamaa yenu, kuomboleza kwenu, bidii yenu kwa ajili yangu; hivi kwamba nikashangilia zaidi tena.

8 Kwa hiyo hata kama niliwahuzunisha ninyi kwa barua yangu,+ mimi sijuti juu ya jambo hilo. Hata kama hapo mwanzoni nilijuta juu ya jambo hilo, (naona kwamba barua hiyo iliwahuzunisha ninyi, ingawa ni kwa kitambo kidogo,) 9 sasa ninashangilia, si kwa sababu mlihuzunishwa tu, bali kwa sababu mlihuzunishwa kufikia kutubu;+ kwa maana mlihuzunishwa kwa njia ya kimungu,+ ili msipatwe na hasara katika jambo lolote kwa sababu yetu. 10 Kwa maana huzuni kwa njia ya kimungu hutokeza toba kuelekea wokovu na haipasi kujuta;+ lakini huzuni ya ulimwengu hutokeza kifo.+ 11 Kwa maana, tazama! jambo hili, kule kuhuzunishwa kwenu kwa njia ya kimungu,+ kulitokeza katika ninyi hali ya bidii kubwa kama nini, ndiyo, kujiondolea wenyewe hatia, ndiyo, ghadhabu, ndiyo, woga, ndiyo, kutamani, ndiyo, bidii, ndiyo, kurekebisha kosa!+ Katika kila jambo mlijionyesha kuwa safi kiadili katika jambo hili. 12 Hakika, ijapokuwa niliwaandikia ninyi, nilifanya hivyo, si kwa ajili ya yeye aliyetenda kosa,+ wala kwa ajili ya yeye aliyekosewa, bali ili bidii yenu kwa ajili yetu ifunuliwe katikati yenu machoni pa Mungu. 13 Ndiyo sababu sisi tumefarijiwa.

Hata hivyo, kwa kuongezea faraja yetu sisi tulishangilia kwa wingi hata zaidi kwa sababu ya shangwe ya Tito, kwa sababu roho+ yake imeburudishwa na ninyi nyote. 14 Kwa maana ikiwa nimejisifu kwake kwa vyovyote juu yenu, sijapata aibu; lakini kama tulivyowaambia mambo yote katika kweli, ndivyo pia kujisifu+ kwetu mbele ya Tito kumekuwa kweli. 15 Pia, upendo wake mwororo ni mwingi zaidi kuwaelekea ninyi, anapokumbuka utii+ wenu nyote, jinsi mlivyompokea kwa kuogopa na kutetemeka. 16 Nashangilia kwamba katika kila njia niwe na uhodari mwingi kwa sababu yenu.+

8 Basi akina ndugu, tunawajulisha ninyi juu ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu ambazo makutaniko ya Makedonia+ yamepewa, 2 kwamba wakati wa jaribu kubwa chini ya mateso shangwe yao nyingi na umaskini mkubwa ulifanya utajiri wa ukarimu wao uwe mwingi.+ 3 Kwa maana hilo lilikuwa kulingana na uwezo wao halisi,+ ndiyo, mimi nashuhudia, kupita uwezo wao halisi, 4 nao kwa kupenda kwao wenyewe waliendelea kutuomba kwa kusihi sana wapate pendeleo la kutoa kwa fadhili na kushiriki katika huduma iliyokusudiwa watakatifu.+ 5 Na si kama tulivyokuwa tumetumaini tu, bali kwanza walijitoa wenyewe kwa Bwana+ na kwetu kupitia mapenzi ya Mungu. 6 Hilo lilituongoza tumtie moyo Tito+ kwamba, kama vile yeye alivyokuwa ameanzisha hilo katikati yenu, vivyo hivyo pia akamilishe utoaji huu wenye fadhili kwa upande wenu. 7 Hata hivyo, kama vile mnavyozidi katika kila jambo,+ katika imani na neno na ujuzi+ na bidii yote na katika upendo huu wetu kwenu, ninyi pia mzidi katika utoaji huu wenye fadhili.

8 Sisemi kwa kuwaamuru ninyi,+ bali ni kwa kufikiria bidii ya wengine na ili kuujaribu uhalisi wa upendo wenu. 9 Kwa maana mnazijua fadhili zisizostahiliwa za Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba ingawa alikuwa tajiri, alikuja kuwa maskini kwa ajili yenu,+ ili muwe matajiri+ kupitia umaskini wake.

10 Na katika jambo hili mimi natoa maoni:+ kwa maana jambo hili ni lenye faida kwenu,+ kwa kuwa tayari mwaka mmoja uliopita mlianzisha si kule kufanya tu bali pia kule kutaka kufanya;+ 11 sasa, basi, malizeni pia kule kufanya hilo, ili, kama vile kulivyokuwa na utayari wa kutaka kufanya, vivyo hivyo pia kuwe kumaliza hilo kutokana na kile mlicho nacho. 12 Kwa maana ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika zaidi kulingana na kile ambacho mtu anacho,+ si kulingana na kile ambacho mtu hana. 13 Kwa maana sikusudii iwe rahisi kwa wengine,+ lakini vigumu kwenu; 14 bali kwamba kupitia usawazisho wa ziada yenu sasa hivi ijazie upungufu wao, ili ziada yao pia ije kujazia upungufu wenu, ili usawazisho uwepo.+ 15 Kama ilivyoandikwa: “Mtu aliyekuwa na vingi hakuwa na vingi mno, na mtu aliyekuwa na vichache hakuwa na vichache mno.”+

16 Basi Mungu na apewe shukrani kwa kuiweka bidii ileile kwa ajili yenu katika moyo wa Tito,+ 17 kwa sababu kwa kweli ameitikia hicho kitia-moyo, lakini, akiwa mwenye bidii sana, anaondoka ili kuja kwenu kwa kupenda kwake mwenyewe. 18 Lakini tunamtuma pamoja naye ndugu ambaye sifa yake kuhusiana na habari njema imeenea katika makutaniko yote. 19 Si hayo tu, bali pia makutaniko yalimweka yeye rasmi+ kuwa mwandamani wetu safarini kuhusiana na zawadi hii ya fadhili ambayo tutaishughulikia kwa ajili ya utukufu+ wa Bwana na kwa uthibitisho wa akili yetu iliyo tayari.+ 20 Hivyo tunaepuka kupata lawama+ kutoka kwa mtu yeyote kuhusiana na mchango+ huu wa ukarimu ambao sisi tutaushughulikia. 21 Kwa maana sisi “tunafanya mpango wa unyoofu, si machoni pa Yehova tu, bali pia machoni pa wanadamu.”+

22 Zaidi ya hayo, tunatuma pamoja nao ndugu yetu ambaye mara nyingi tumemjaribu tukaona katika mambo mengi ana bidii, lakini sasa ni mwenye bidii nyingi zaidi kwa sababu ya uhakika wake mkubwa katika ninyi. 23 Ingawa hivyo, kama kuna swali lolote kumhusu Tito, yeye ni mshiriki pamoja nami na mfanyakazi mwenzangu+ kwa ajili ya faida yenu; au kama ni kuhusu ndugu zetu, wao ni mitume wa makutaniko na utukufu wa Kristo. 24 Kwa hiyo waonyesheni uthibitisho wa upendo+ wenu na wa yale tuliyojisifu+ juu yenu, mbele ya makutaniko.

9 Basi kuhusu huduma+ ambayo ni kwa ajili ya watakatifu, ni jambo la ziada mimi kuwaandikia ninyi, 2 kwa maana naujua utayari wenu wa akili ambao najisifia kwa Wamakedonia juu yenu, kwamba Akaya imesimama tayari kwa mwaka mmoja+ sasa, na bidii yenu imewachochea walio wengi kati yao. 3 Lakini ninawatuma akina ndugu, ili kujisifu kwetu juu yenu kusiwe kwa bure kwa habari hii, bali ili muwe tayari kwelikweli,+ kama nilivyokuwa nikisema mngekuwa. 4 Kama sivyo, kwa njia fulani, Wamakedonia wakija pamoja nami na kuwakuta mkiwa hamko tayari, sisi—sisemi ninyi—tutaona aibu katika huu uhakikisho wetu. 5 Kwa hiyo niliona kuwa ni jambo la lazima niwatie moyo akina ndugu watangulie kuja kwenu na kuitayarisha mapema zawadi yenu ya ukarimu iliyoahidiwa hapo mwanzoni,+ ili kwamba hiyo iwe tayari kama zawadi ya ukarimu na si kama kitu kilichopatikana kwa kunyang’anywa.+

6 Lakini kuhusu hili, yeye anayepanda kwa uhaba+ atavuna pia kwa uhaba; na yeye anayepanda kwa wingi+ atavuna pia kwa wingi. 7 Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda+ wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.+

8 Zaidi ya hayo, Mungu anaweza kufanya fadhili zake zote zisizostahiliwa ziwe nyingi kuwaelekea ninyi, ili, ijapokuwa sikuzote mna ujitoshelevu kamili katika kila kitu, muwe na vingi kwa ajili ya kila kazi njema.+ 9 (Kama ilivyoandikwa: “Amegawa kwa wingi, amewapa maskini, uadilifu wake unaendelea milele.”+ 10 Basi yeye ambaye humgawia mpandaji wa mbegu kwa wingi na mkate wa kula+ atawagawia na kuwazidishia ninyi mbegu ili mpande naye ataongeza mazao ya uadilifu wenu.)+ 11 Katika kila kitu mnatajirishwa kwa ajili ya kila namna ya ukarimu, ambao hutokeza kupitia sisi wonyesho wa shukrani kwa Mungu;+ 12 kwa sababu huduma ya utumishi huu wa watu wote si kugawa tu kwa wingi mahitaji ya watakatifu+ bali pia kuwa matajiri kwa maonyesho mengi ya shukrani kwa Mungu. 13 Kupitia uthibitisho ambao huduma hii hutoa, wao wanamtukuza Mungu kwa sababu mnajitiisha kwenye habari njema juu ya Kristo,+ mnapotangaza waziwazi kuwa mko hivyo, na kwa sababu ninyi ni wakarimu katika mchango wenu kwao na kwa wote;+ 14 nao kupitia dua kwa ajili yenu wanatamani kuwaona ninyi kwa sababu ya fadhili nyingi zaidi zisizostahiliwa+ za Mungu juu yenu.

15 Mungu apewe shukrani kwa ajili ya zawadi yake ya bure isiyoelezeka.+

10 Basi mimi mwenyewe, Paulo, nawasihi ninyi kwa upole+ na fadhili+ za Kristo, ingawa kuonekana kwangu+ katikati yenu ni kwa hali ya chini, lakini nisipokuwapo mimi ni jasiri kuwaelekea ninyi.+ 2 Kwa kweli naomba kwamba, nitakapokuwapo, nisitumie ujasiri kwa uhakika ule ambao nategemea kuchukua hatua za kijasiri+ juu ya wengine ambao wanatukadiria sisi kana kwamba tulitembea kulingana na tulivyo katika mwili. 3 Kwa maana ingawa tunatembea katika mwili,+ hatupigi vita kulingana na tulivyo katika mwili.+ 4 Kwa maana silaha za vita vyetu si za kimwili,+ bali ni zenye nguvu kwa Mungu+ kwa ajili ya kupindua ngome zenye nguvu. 5 Kwa maana sisi tunapindua mawazo na kila jambo lililo juu sana ambalo limeinuliwa kinyume cha ujuzi wa Mungu;+ nasi tunaiteka kila fikira ili kuifanya imtii Kristo; 6 nasi tuko tayari kutoa adhabu kwa ajili ya kila kitu kisichotii,+ mara tu utii wenu wenyewe utakapokuwa umeisha kutimizwa kikamilifu.+

7 Mnayatazama mambo kulingana na thamani yake ya juujuu.+ Mtu yeyote akijitegemea mwenyewe kwamba ni wa Kristo, acheni yeye atie akilini tena jambo hili kwa ajili yake mwenyewe, kwamba, kama vile yeye alivyo wa Kristo, ndivyo na sisi pia.+ 8 Kwa maana hata nikijisifu+ mno kidogo juu ya mamlaka ambayo Bwana alitupa sisi ili tuwajenge wala si kuwabomoa ninyi,+ mimi sitaaibishwa, 9 ili nisionekane kuwa nataka kuwatia ninyi hofu kwa barua zangu. 10 Kwa maana, wao husema: “Barua zake ni nzito na zenye nguvu nyingi, lakini kuwapo kwake mwenyewe kimwili ni dhaifu+ na maneno yake ni yenye kudharaulika.”+ 11 Mtu wa namna hiyo na atie jambo hili akilini, kwamba kile tulicho katika neno letu kwa barua wakati hatupo, ndivyo tutakavyokuwa pia katika tendo tutakapokuwapo.+ 12 Kwa maana sisi hatuthubutu kujiweka katika kikundi cha watu fulani au kujilinganisha na watu fulani ambao hujipendekeza wenyewe.+ Hakika wao kwa kujipima wenyewe kwa wenyewe na kujilinganisha wenyewe kwa wenyewe, hawana uelewaji.+

13 Kwa upande wetu sisi tutajisifu, si nje ya mipaka yetu tuliyogawiwa,+ bali kulingana na mpaka wa eneo ambalo Mungu alitugawia kwa kipimio, akilifanya lifike hadi kwenu.+ 14 Kwa kweli sisi hatujinyooshi wenyewe kupita kiasi kana kwamba hatukuwafikia ninyi, kwa maana sisi tulikuwa wa kwanza kuja hadi kwenu katika kutangaza habari njema juu ya Kristo.+ 15 Hapana, hatujisifu katika kazi za jasho za mtu mwingine nje ya mipaka yetu tuliyogawiwa,+ bali tunatumainia kwamba, kadiri imani yenu inavyoongezwa,+ ndivyo sisi tutakavyofanywa wakubwa katikati yenu kuhusiana na eneo letu.+ Ndipo tutakapozidi hata zaidi, 16 kutangaza habari njema kwenye nchi zilizo ng’ambo yenu,+ ili tusijisifu katika eneo la mtu mwingine ambapo mambo yamekwisha kutayarishwa. 17 “Bali yeye anayejisifu, na ajisifu katika Yehova.”+ 18 Kwa maana yule anayejipendekeza si ndiye ambaye hukubaliwa,+ bali ni yule mtu ambaye Yehova+ humpendekeza.+

11 Laiti mngenivumilia katika kukosa kidogo akili.+ Lakini, kwa kweli, ninyi mnanivumilia! 2 Kwa maana nina wivu juu yenu kwa wivu wa kimungu,+ kwa maana mimi binafsi niliwachumbia+ ninyi mume+ mmoja ili niwatoe mkiwa bikira safi kiadili+ kwa Kristo.+ 3 Lakini naogopa kwamba kwa njia fulani, kama nyoka alivyomshawishi Hawa+ kwa ujanja wake, huenda akili zenu zikaharibiwa+ kutoka kwenye unyoofu wa moyo na usafi wa kiadili ambao unamfaa Kristo.+ 4 Kwa maana, kama ilivyo, mtu fulani akija na kuhubiri Yesu mwingine tofauti na yule tuliyemhubiri,+ au mkipokea roho nyingine tofauti na ile mliyopokea,+ au habari njema+ nyingine tofauti na ile mliyokubali, mnamvumilia kwa urahisi.+ 5 Kwa maana naona kwamba hata katika jambo moja sijawa mdogo+ kwa mitume wenu walio bora sana.+ 6 Lakini hata kama sina ustadi wa kusema,+ hakika sivyo nilivyo katika ujuzi;+ lakini katika kila njia tuliwafunulia ninyi hilo katika mambo yote.+

7 Au je, nilifanya dhambi kwa kujinyenyekeza+ ili ninyi mwinuliwe, kwa sababu niliwatangazia ninyi habari njema ya Mungu kwa furaha bila gharama?+ 8 Niliyanyang’anya makutaniko mengine kwa kupokea vitu kutoka kwao ili niwahudumie ninyi;+ 9 na bado nilipokuwa pamoja nanyi na nikapatwa na uhitaji, sikuwa mzigo kwa mtu hata mmoja,+ kwa maana ndugu waliotoka Makedonia+ walijazia kwa wingi upungufu wangu. Ndiyo, katika kila njia nilikaa mwenyewe bila kuwa mzigo kwenu nami nitakaa hivyo.+ 10 Ni kweli+ ya Kristo katika hali yangu kwamba huku kujisifu+ kwangu hakutakomeshwa katika maeneo ya Akaya. 11 Kwa sababu gani? Je, ni kwa sababu siwapendi ninyi? Mungu anajua ninawapenda.+

12 Basi lile ninalofanya bado mimi nitalifanya,+ ili nikatilie mbali kisingizio kutoka kwa wale wanaotaka kisingizio cha kupatikana kuwa sawa nasi katika cheo ambacho wanajisifia. 13 Kwa maana watu wa namna hiyo ni mitume wa uwongo, wafanyakazi wadanganyifu,+ wakijigeuza wenyewe kuwa mitume wa Kristo.+ 14 Na si ajabu, kwa maana Shetani mwenyewe huendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru.+ 15 Kwa hiyo si jambo kubwa kama wahudumu+ wake wakiendelea pia kujigeuza wenyewe kuwa wahudumu wa uadilifu. Lakini mwisho wao utakuwa kulingana na matendo yao.+

16 Nasema tena, Mtu yeyote asifikiri kwamba mimi sina akili. Na bado, ikiwa kwa kweli mnafikiri hivyo, mnikubali hata ikiwa ni kana kwamba sina akili, ili mimi vilevile nijisifu+ kidogo kwa kiasi fulani. 17 Lile ninalosema nalisema, si kwa kufuata kielelezo cha Bwana, bali kama katika ukosefu wa akili, katika uhakika huu wa kupita kiasi ulio kawaida ya kujisifu.+ 18 Kwa kuwa wengi wanajisifu kulingana na mwili,+ mimi pia nitajisifu. 19 Kwa maana ninyi mnawavumilia kwa furaha watu wasio na akili, kwa kuwa ninyi mna akili. 20 Kwa kweli, mnamvumilia yeyote anayewafanya ninyi kuwa watumwa,+ yeyote anayemeza kile mlicho nacho, yeyote anayenyakua kile mlicho nacho, yeyote anayejiinua mwenyewe juu yenu, yeyote anayewapiga usoni.+

21 Nasema hili kwa aibu yetu, kana kwamba cheo chetu ni dhaifu.

Lakini mtu mwingine yeyote akitenda kwa ujasiri katika jambo fulani—mimi ninaongea kwa kukosa akili+—mimi pia ninatenda kwa ujasiri katika jambo hilo. 22 Je, wao ni Waebrania? Mimi pia.+ Je, wao ni Waisraeli? Mimi pia. Je, wao ni uzao wa Abrahamu? Mimi pia.+ 23 Je, wao ni wahudumu wa Kristo? Mimi najibu kama mwenda-wazimu, mimi ni mhudumu kwa njia yenye kutokeza hata zaidi:+ katika kazi za jasho kwa wingi zaidi,+ katika vifungo vya gereza kwa wingi zaidi,+ katika mapigo kwa kuzidi mno, katika kukaribia kufa mara nyingi.+ 24 Kwa Wayahudi nilipokea mara tano mapigo 40+ kupungua moja, 25 mara tatu nilipigwa kwa fimbo,+ mara moja nilipigwa kwa mawe,+ mara tatu nilivunjikiwa na meli,+ usiku mmoja na mchana mmoja nimekaa katika kilindi; 26 katika safari mara nyingi, katika hatari za kutokana na mito, katika hatari za kutokana na wanyang’anyi wa njia kuu,+ katika hatari za kutokana na jamii yangu+ mwenyewe, katika hatari za kutokana na mataifa,+ katika hatari ndani ya jiji,+ katika hatari za nyikani, katika hatari za baharini, katika hatari za katikati ya ndugu wa uwongo, 27 katika kazi ya jasho na kutaabika, katika usiku mwingi bila usingizi+ mara nyingi, katika njaa na kiu,+ katika kuepukana na chakula+ nyakati nyingi, katika baridi na uchi.

28 Mbali na mambo hayo ya aina ya nje, kuna kinachonikaza ndani siku kwa siku, hangaiko kwa ajili ya makutaniko yote.+ 29 Ni nani aliye dhaifu,+ nami si dhaifu? Ni nani amekwazika, nami siwaki hasira?

30 Ikiwa ni lazima kujisifu, mimi nitajisifu+ juu ya mambo yanayohusiana na udhaifu wangu. 31 Mungu na Baba ya Bwana Yesu, naam, Yeye aliye wa kusifiwa milele, anajua sisemi uwongo. 32 Katika Damasko gavana aliye chini ya Areta mfalme alikuwa akilinda jiji la Wadamasko ili kunikamata,+ 33 lakini nilishushwa kupitia dirisha ukutani katika kapu+ kubwa nami nikaiponyoka mikono yake.

12 Lazima nijisifu. Haina faida; lakini nitaendelea katika maono+ ya miujiza na ufunuo wa Bwana. 2 Namjua mtu mmoja katika muungano na Kristo ambaye, miaka kumi na minne iliyopita—kama ni katika mwili sijui, au ni nje ya mwili sijui; Mungu anajua—alinyakuliwa+ akiwa hivyo mpaka kwenye mbingu ya tatu. 3 Ndiyo, namjua mtu wa namna hiyo—kama ni katika mwili au bila mwili,+ mimi sijui, Mungu anajua— 4 kwamba alinyakuliwa kuingia katika paradiso+ na kusikia maneno yasiyoweza kutamkwa ambayo si halali mtu kuyasema. 5 Mimi nitajisifu juu ya mtu wa namna hiyo, lakini mimi sitajisifu juu yangu mwenyewe, isipokuwa kwa habari ya udhaifu wangu.+ 6 Kwa maana hata nikitaka kujisifu,+ sitakuwa mwenye kukosa akili, kwa maana nitasema kweli. Lakini naepuka, ili yeyote asinihesabie sifa zaidi ya kile anachoniona mimi kuwa au anachosikia kutoka kwangu, 7 kwa sababu tu ya wingi wa huo ufunuo.

Kwa hiyo, ili nisijione kuwa nimeinuliwa mno,+ nilipewa mwiba katika mwili,+ malaika wa Shetani, aendelee kunipiga kofi, ili nisijiinue kupita kiasi. 8 Kwa ajili ya hilo mara tatu+ nilimsihi Bwana kwamba huo uniondoke; 9 na bado kwa kweli akaniambia: “Fadhili zangu zisizostahiliwa zinakutosha+ wewe; kwa maana nguvu zangu zinakamilishwa katika udhaifu.”+ Kwa furaha zaidi, basi, ni afadhali nijisifu kwa habari ya udhaifu wangu,+ ili nguvu za Kristo zibaki juu yangu kama hema. 10 Kwa hiyo napendezwa na udhaifu, na matusi, na hali za uhitaji, na mateso na magumu, kwa ajili ya Kristo. Kwa maana ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa mwenye nguvu.+

11 Nimekuwa mtu asiye na akili. Ninyi mlinilazimisha+ kuwa hivyo, kwa maana ninyi mlipaswa kunipendekeza. Kwa maana hata katika jambo moja sikuwa mdogo kwa mitume wenu walio bora sana,+ hata kama mimi si kitu.+ 12 Kwa kweli, ishara za mtume+ zilitokezwa katikati yenu kwa uvumilivu wote,+ na kwa ishara na mambo ya ajabu na matendo yenye nguvu.+ 13 Kwa maana ni katika jambo gani kwamba ninyi mlikuwa wadogo kuliko yale makutaniko mengine, isipokuwa kwamba mimi mwenyewe sikuwa mzigo kwenu?+ Mnisamehe kosa hili kwa fadhili.

14 Tazama! Hii ndiyo mara ya tatu+ niliyo tayari kuja kwenu, na bado sitakuwa mzigo. Kwa maana ninatafuta, si mali zenu,+ bali ninyi; kwa maana watoto+ hawapaswi kuweka akiba kwa ajili ya wazazi wao, bali wazazi kwa ajili ya watoto wao.+ 15 Kwa upande wangu mimi nitatumia kwa furaha zaidi na kutumiwa kabisa kwa ajili ya nafsi zenu.+ Kama nikiwapenda ninyi kwa wingi zaidi, je, mimi nipendwe kidogo? 16 Lakini hata iweje, mimi sikuwa mzigo mzito kwenu.+ Hata hivyo ninyi mnasema, mimi nilikuwa “mjanja” nami niliwashika ninyi “kwa ujanja.”+ 17 Kwa habari ya yeyote kati ya wale niliowatuma kwenu, je, niliwatumia ninyi kwa kujifaidi kupitia yeye? 18 Nilimhimiza Tito na nikamtuma yule ndugu pamoja naye. Je, Tito aliwatumia ninyi kwa kujifaidi hata kidogo?+ Je, hatukutembea katika roho ileile?+ Katika hatua zilezile?

19 Je, ninyi mmekuwa mkifikiri muda huu wote kwamba sisi tumekuwa tukijitetea kwenu? Sisi tunasema mbele za Mungu kuhusiana na Kristo. Lakini, wapendwa, mambo yote ni kwa ajili ya kuwajenga ninyi.+ 20 Kwa maana naogopa kwamba kwa njia fulani, nitakapofika,+ huenda nikawapata ninyi mkiwa vile ambavyo mimi sipendi nami niwe kwenu vile ambavyo ninyi hampendi, bali, badala yake, kwa njia fulani inaelekea kutakuwa na mizozo, wivu,+ milipuko ya hasira, magomvi, masengenyo, manong’onezo, majivuno, machafuko.+ 21 Labda, nitakapokuja tena, huenda Mungu wangu akaninyenyekeza katikati yenu, nami huenda nikaomboleza juu ya wengi kati ya wale ambao hapo zamani walitenda dhambi+ lakini hawajatubu kutokana na unajisi wao na uasherati+ na mwenendo mpotovu+ ambao wamezoea kutenda.

13 Hii ndiyo mara ya tatu+ ambayo ninakuja kwenu. “Kwa kinywa cha mashahidi wawili au cha watatu kila jambo litathibitishwa.”+ 2 Nimesema hapo mwanzoni na, kana kwamba nipo mara ya pili lakini sipo sasa, nawaambia kimbele wale ambao wametenda dhambi hapo mwanzoni na kwa wengine wote, kwamba ikiwa nitakuja tena sitahurumia,+ 3 kwa kuwa mnatafuta uthibitisho wa Kristo akisema ndani yangu,+ Kristo ambaye si dhaifu kuwaelekea ninyi bali ni mwenye nguvu kati yenu. 4 Ni kweli, yeye alitundikwa mtini+ kwa sababu ya udhaifu,+ lakini yeye yuko hai kwa sababu ya nguvu za Mungu.+ Ni kweli, pia, sisi ni dhaifu pamoja naye,+ lakini tutaishi pamoja naye kwa sababu ya nguvu za Mungu+ kuwaelekea ninyi.

5 Endeleeni kujijaribu kama ninyi mko katika imani, endeleeni kuthibitisha ninyi wenyewe jinsi mlivyo.+ Au je, hamtambui kwamba Yesu Kristo yumo katika muungano pamoja na ninyi?+ Isipokuwa muwe mmekataliwa. 6 Kwa kweli natumaini mtajua kwamba sisi hatujakataliwa.

7 Basi tunasali+ kwa Mungu kwamba msifanye kosa, si kwamba sisi wenyewe tuonekane kuwa waliokubaliwa, bali kwamba muwe mkifanya yaliyo mazuri, ingawa sisi wenyewe huenda tukaonekana kuwa waliokataliwa. 8 Kwa maana hatuwezi kufanya jambo lolote kinyume cha kweli, bali kwa ajili ya kweli.+ 9 Hakika sisi hushangilia wakati wowote tunapokuwa dhaifu lakini ninyi ni wenye nguvu;+ nasi tunasali+ kwa ajili ya jambo hili, mrekebishwe upya. 10 Hiyo ndiyo sababu naandika mambo haya nikiwa sipo, ili, nitakapokuwapo, nisitende kwa ukali+ kulingana na mamlaka ambayo Bwana alinipa, ili kujenga+ na si kubomoa.

11 Mwishowe, akina ndugu, endeleeni kushangilia, kurekebishwa upya, kufarijiwa,+ kufikiri kwa upatano,+ kuishi kwa amani;+ na Mungu wa upendo na wa amani+ atakuwa pamoja nanyi. 12 Salimianeni kwa busu takatifu.+ 13 Watakatifu wote wanawatumia ninyi salamu zao.

14 Fadhili zisizostahiliwa za Bwana Yesu Kristo na upendo wa Mungu na ushirika katika roho takatifu ziwe pamoja na ninyi nyote.+

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki