DANIELI
1 Katika mwaka wa tatu wa utawala wa Mfalme Yehoyakimu+ wa Yuda, Mfalme Nebukadneza wa Babiloni alikuja na kuzingira Yerusalemu.+ 2 Baada ya muda Yehova akamtia Mfalme Yehoyakimu wa Yuda mikononi mwake,+ pamoja na baadhi ya vyombo vya nyumba ya* Mungu wa kweli, akavileta katika nchi ya Shinari*+ katika nyumba ya* mungu wake. Akaviweka katika hazina ya mungu wake.+
3 Kisha Mfalme Nebukadneza akamwagiza Ashpenazi ofisa mkuu wa makao yake ya kifalme awalete baadhi ya Waisraeli,* kutia ndani wale wanaotoka katika uzao wa kifalme na wa watu mashuhuri.+ 4 Walipaswa kuwa vijana* wasio na kasoro yoyote, wazuri kwa umbo, waliobarikiwa kuwa na hekima, ujuzi, na utambuzi,+ na wanaoweza kutumikia katika jumba la mfalme. Alipaswa kuwafundisha maandishi na lugha ya Wakaldayo. 5 Pia, mfalme aliagiza wapewe kila siku vyakula bora ambavyo yeye mwenyewe alikula na divai ambayo alikunywa. Walipaswa kuzoezwa* kwa miaka mitatu, na baada ya muda huo wangeanza kumtumikia mfalme.
6 Sasa baadhi ya vijana hao walikuwa wa kabila la* Yuda: Danieli,*+ Hanania,* Mishaeli,* na Azaria.*+ 7 Na ofisa mkuu wa makao ya mfalme akawapa majina;* alimpa Danieli jina Belteshaza,+ akampa Hanania jina Shadraki, akampa Mishaeli jina Meshaki, na kumpa Azaria jina Abednego.+
8 Lakini Danieli aliazimia moyoni mwake kwamba hatajichafua kwa vyakula bora vya mfalme wala divai yake. Basi akamwomba ofisa mkuu wa makao ya mfalme ruhusa ya kutojichafua kwa njia hiyo. 9 Na Mungu wa kweli akamfanya ofisa mkuu wa makao ya mfalme amtendee Danieli kwa fadhili* na rehema.+ 10 Lakini ofisa mkuu wa makao ya mfalme akamwambia Danieli: “Ninamwogopa bwana wangu mfalme, ambaye ametoa maagizo kuhusu vyakula na vinywaji vyenu. Itakuwaje akiona kwamba afya yenu ni mbaya kuliko ya vijana* wengine wa rika lenu? Mtanifanya niwe na* hatia mbele ya mfalme.” 11 Lakini Danieli akamwambia mtu aliyeteuliwa na ofisa mkuu wa makao ya mfalme ili kumtunza yeye, Hanania, Mishaeli, na Azaria: 12 “Tafadhali, tujaribu sisi watumishi wako kwa siku kumi, tupe mboga za majani na maji ya kunywa; 13 kisha linganisha sura zetu na sura za vijana* wanaokula vyakula bora vya mfalme, halafu ututendee sisi watumishi wako kulingana na jinsi tunavyoonekana machoni pako.”
14 Basi akakubali pendekezo lao na kuwajaribu kwa siku kumi. 15 Baada ya siku kumi sura yao ilikuwa nzuri zaidi na yenye afya zaidi* kuliko ya vijana* wote waliokuwa wakila vyakula bora vya mfalme. 16 Kwa hiyo mtu aliyewatunza alikuwa akichukua vyakula vyao bora na divai yao na kuwapa mboga za majani. 17 Na Mungu wa kweli aliwapa vijana* hao wanne ujuzi na ufahamu wa kila aina ya maandishi na hekima; naye Danieli alipewa uwezo wa kuelewa maono na ndoto za kila aina.+
18 Mwishoni mwa kipindi ambacho mfalme aliagiza vijana wote waletwe ndani,+ ofisa mkuu wa makao ya mfalme aliwaleta mbele ya Nebukadneza. 19 Mfalme alipozungumza nao, hakuna kijana yeyote katika kikundi chote aliyekuwa kama Danieli, Hanania, Mishaeli, na Azaria;+ nao wakaendelea kumtumikia mfalme. 20 Katika kila jambo lililohitaji hekima na uelewaji ambalo mfalme aliwauliza, aliona kwamba walikuwa bora mara kumi kuliko makuhani wote wachawi na watu waliofanya mazingaombwe+ katika milki yake yote. 21 Danieli alibaki huko mpaka mwaka wa kwanza wa Mfalme Koreshi.+
2 Katika mwaka wa pili wa utawala wake, Nebukadneza aliota ndoto kadhaa, akahangaika* sana+ hivi kwamba akashindwa kulala. 2 Basi mfalme akaagiza makuhani wachawi, watu wanaofanya mazingaombwe, walozi, na Wakaldayo* waitwe ili wamwambie mfalme ndoto zake. Kwa hiyo wakaja na kusimama mbele ya mfalme.+ 3 Kisha mfalme akawaambia: “Nimeota ndoto, nami ninahangaika* kwa sababu ninataka kujua nilichoota.” 4 Wakaldayo wakamjibu mfalme kwa lugha ya Kiaramu:*+ “Ee mfalme, na uishi milele. Tusimulie ndoto yako sisi watumishi wako, nasi tutakuambia maana yake.”
5 Mfalme akawajibu Wakaldayo: “Nimeamua hivi: Msiponiambia ndoto yangu na kunieleza maana yake, mtakatwa vipandevipande, na nyumba zenu zitageuzwa kuwa vyoo vya umma.* 6 Lakini mkiniambia ndoto yangu na kunieleza maana yake, nitawapa zawadi na tuzo na heshima kubwa.+ Basi niambieni ndoto hiyo na maana yake.”
7 Wakamjibu kwa mara ya pili: “Ee mfalme, tuambie ndoto yako, sisi watumishi wako, nasi tutakueleza maana yake.”
8 Mfalme akawajibu: “Najua vema kwamba mnajaribu kujipatia muda, kwa kuwa mnajua uamuzi wangu. 9 Msiponiambia ndoto yangu, adhabu yenu nyote ni moja tu. Lakini mmekubaliana kunidanganya na kunihadaa, mkitumaini kwamba hali itabadilika. Basi niambieni ndoto hiyo, nami nitajua kwamba mnaweza kueleza maana yake.”
10 Wakaldayo wakamjibu mfalme: “Hakuna mtu yeyote duniani* anayeweza kufanya jambo ambalo wewe mfalme unaagiza, kwa sababu hakuna mfalme yeyote mkuu wala gavana aliyewahi kumwomba kuhani yeyote mchawi, au mtu yeyote anayefanya mazingaombwe, au Mkaldayo afanye jambo kama hili. 11 Jambo ambalo wewe mfalme unaomba ni gumu, na hakuna yeyote anayeweza kukwambia jambo hilo isipokuwa miungu, ambao hawaishi miongoni mwa wanadamu.”*
12 Ndipo mfalme akashikwa na ghadhabu kali, akaagiza wanaume wote wenye hekima wa Babiloni waangamizwe.+ 13 Agizo hilo lilipotolewa na wakati ulipokaribia wa kuwaua wanaume hao wenye hekima, walimtafuta pia Danieli na wenzake ili wawaue.
14 Wakati huo, kwa busara na tahadhari Danieli alizungumza na Arioko mkuu wa walinzi wa mfalme, alipokuwa akienda kuwaua wanaume wenye hekima wa Babiloni. 15 Akamuuliza Arioko ofisa wa mfalme: “Kwa nini mfalme ametoa agizo kali hivyo?” Ndipo Arioko akamweleza Danieli jambo hilo.+ 16 Basi Danieli akaenda na kumwomba mfalme ampe muda ili amweleze maana ya ndoto yake.
17 Kisha Danieli akarudi nyumbani kwake na kuwajulisha wenzake, Hanania, Mishaeli, na Azaria kuhusu jambo hilo. 18 Akawaambia wasali ili Mungu wa mbinguni awaonyeshe rehema na kuwajulisha siri hiyo, ili yeye Danieli, na wenzake wasiangamizwe pamoja na wale wanaume wengine wenye hekima wa Babiloni.
19 Kisha Danieli akafunuliwa siri hiyo katika maono wakati wa usiku.+ Basi Danieli akamsifu Mungu wa mbinguni. 20 Danieli akasema:
21 Yeye hubadili nyakati na majira,+
Huwaondoa wafalme na kuwaweka wafalme,+
Huwapa hekima walio na hekima na kuwapa ujuzi wale walio na utambuzi.+
22 Yeye hufunua mambo yenye kina na mambo yaliyofichika,+
23 Ee Mungu wa mababu zangu, ninakushukuru na kukusifu,
Kwa sababu umenipa hekima na nguvu.
Na sasa umenijulisha tulichokuomba;
Umetujulisha jambo linalomhangaisha mfalme.”+
24 Kisha Danieli akaenda kwa Arioko, ambaye alikuwa ameteuliwa na mfalme kuwaangamiza wanaume wenye hekima wa Babiloni,+ akamwambia: “Usimwangamize mwanamume yeyote mwenye hekima wa Babiloni. Nipeleke mbele ya mfalme, nami nitamweleza mfalme maana ya ndoto yake.”
25 Mara moja Arioko akampeleka Danieli mbele ya mfalme na kumwambia: “Nimempata mwanamume fulani miongoni mwa watu waliohamishwa kutoka Yuda+ anayeweza kukueleza maana ya ndoto yako.” 26 Mfalme akamuuliza Danieli, aliyeitwa Belteshaza:+ “Je, kweli unaweza kuniambia ndoto niliyoota, na maana yake?”+ 27 Danieli akamjibu mfalme: “Hakuna mwanamume yeyote mwenye hekima, wala mtu anayefanya mazingaombwe, wala kuhani yeyote mchawi, wala mnajimu yeyote anayeweza kukufunulia wewe mfalme siri unayoomba ifunuliwe.+ 28 Lakini kuna Mungu mbinguni ambaye ni Mfunuaji wa siri,+ naye amekujulisha wewe Mfalme Nebukadneza mambo yatakayotukia katika kipindi cha mwisho cha zile siku. Hii ndiyo ndoto yako, na haya ndiyo maono yaliyokujia kichwani ulipokuwa umelala kitandani:
29 “Ee mfalme, ulipokuwa kitandani uliona katika mawazo yako mambo yatakayotukia wakati ujao, na Mfunuaji wa siri amekujulisha mambo yatakayotukia. 30 Lakini siri hii imefunuliwa kwangu si kwa sababu nina hekima nyingi zaidi kuliko mtu yeyote anayeishi, bali ilifunuliwa kwangu ili nikueleze wewe mfalme maana ya ndoto yako ili ujue mawazo yaliyo moyoni mwako.+
31 “Wewe, Ee mfalme, ulitazama na kuona sanamu kubwa sana. Sanamu hiyo, iliyokuwa kubwa sana na iliyong’aa kupita kiasi, ilisimama mbele yako, nayo ilikuwa yenye kutisha. 32 Kichwa cha sanamu hiyo kilikuwa cha dhahabu bora,+ kifua chake na mikono yake ilikuwa ya fedha,+ tumbo na mapaja yake yalikuwa ya shaba,+ 33 miguu yake ilikuwa ya chuma,+ na kwa sehemu, nyayo zake zilikuwa za chuma na kwa sehemu zilikuwa za udongo wa mfinyanzi.*+ 34 Uliendelea kutazama hadi jiwe likakatwa, si kwa mikono, nalo likaipiga sanamu hiyo kwenye nyayo zake za chuma na za udongo wa mfinyanzi na kuzipondaponda.+ 35 Wakati huo kile chuma, ule udongo wa mfinyanzi, ile shaba, ile fedha, na ile dhahabu, vyote pamoja, vikapondwapondwa na kuwa kama makapi kutoka kwenye uwanja wa kupuria wakati wa kiangazi, kisha upepo ukavipeperusha mbali hivi kwamba hakuna chembe yoyote ya vitu hivyo ingeweza kupatikana. Lakini lile jiwe lililoipiga ile sanamu likawa mlima mkubwa, nalo likaijaza dunia yote.
36 “Hiyo ndiyo ndoto yako, na sasa tutakueleza maana yake. 37 Wewe, Ee mfalme—mfalme wa wafalme ambaye Mungu wa mbinguni amekupa ufalme,+ uwezo, nguvu, na utukufu, 38 na kuwaweka mikononi mwako wanadamu mahali popote ambapo huenda wanaishi, na pia wanyama wa mwituni na ndege wa angani, na kukufanya kuwa mtawala juu ya hao wote+—wewe mwenyewe ndiye kichwa cha dhahabu.+
39 “Lakini baada yako ufalme mwingine utainuka,+ ulio dhaifu kwako; kisha ufalme mwingine, wa tatu, wa shaba, ambao utaitawala dunia yote.+
40 “Ufalme wa nne utakuwa wenye nguvu kama chuma.+ Kwa maana kama vile chuma kinavyopondaponda na kusagasaga vitu vingine vyote, naam, kama chuma kinachovunjavunja, ufalme huo utapondaponda na kuzivunjavunja falme hizo zote.+
41 “Na kama tu ulivyoona kwamba nyayo na vidole vya miguu kwa sehemu vilikuwa vya udongo wa mfinyanzi na kwa sehemu vilikuwa vya chuma, ufalme huo utagawanyika, lakini ugumu fulani wa chuma utakuwa ndani yake, kama tu ulivyoona chuma kikiwa kimechanganyika na udongo laini wa mfinyanzi. 42 Na kama vile vidole vyake vya miguu vilikuwa kwa sehemu vya chuma na kwa sehemu vya udongo wa mfinyanzi, ndivyo ufalme huo utakavyokuwa na nguvu kwa sehemu na kuwa dhaifu kwa sehemu. 43 Kama tu ulivyoona chuma kikiwa kimechanganyika na udongo laini wa mfinyanzi, sehemu hizo zitachanganyika na wanadamu;* lakini hazitashikamana na wanadamu, kama tu chuma kisivyochanganyika na udongo wa mfinyanzi.
44 “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme+ ambao hautaangamizwa kamwe.+ Na ufalme huo hautakabidhiwa watu wengine wowote.+ Utazipondaponda na kuzikomesha falme hizi zote,+ nao pekee utasimama milele,+ 45 kama tu ulivyoona kwamba jiwe ambalo halikukatwa kwa mikono lilitoka kwenye mlima, na kwamba lilipondaponda kile chuma, ile shaba, ule udongo wa mfinyanzi, ile fedha, na ile dhahabu.+ Mungu Mtukufu amemjulisha mfalme mambo yatakayotukia wakati ujao.+ Ndoto hiyo ni ya kweli, na maana yake inategemeka.”
46 Ndipo Mfalme Nebukadneza akaanguka chini kifudifudi mbele ya Danieli na kumpa heshima kubwa. Naye akaagiza apewe zawadi na kufukiziwa uvumba. 47 Mfalme akamwambia Danieli: “Kwa kweli Mungu wako ni Mungu wa miungu na Bwana wa wafalme na Mfunuaji wa siri, kwa sababu uliweza kufunua siri hii.”+ 48 Kisha mfalme akampandisha cheo Danieli na kumpa zawadi nyingi bora, naye akamfanya kuwa mtawala wa mkoa wote wa* Babiloni+ na msimamizi mkuu wa wanaume wote wenye hekima wa Babiloni. 49 Na kwa ombi la Danieli, mfalme akawaweka Shadraki, Meshaki, na Abednego+ kuwa wakuu wa usimamizi wa mkoa wa* Babiloni, lakini Danieli alifanya kazi katika makao ya mfalme.
3 Mfalme Nebukadneza alitengeneza sanamu ya dhahabu yenye urefu wa mikono 60* na upana wa mikono 6.* Akaisimamisha kwenye nchi tambarare ya Dura katika mkoa wa* Babiloni. 2 Kisha Mfalme Nebukadneza akatuma ujumbe ili kuwakusanya maliwali, wasimamizi, magavana, washauri, watunza-hazina, waamuzi, mahakimu, na wasimamizi wote wa mikoa* waje kwenye sherehe ya kuzindua sanamu ambayo Mfalme Nebukadneza alikuwa amesimamisha.
3 Basi maliwali, wasimamizi, magavana, washauri, watunza-hazina, waamuzi, mahakimu, na wakuu wote wa mikoa* wakakusanyika kwa ajili ya sherehe ya kuzindua sanamu ambayo Mfalme Nebukadneza alikuwa amesimamisha. Nao wakasimama mbele ya sanamu iliyosimamishwa na Nebukadneza. 4 Mpiga mbiu akatangaza hivi kwa sauti kubwa: “Enyi watu wa makabila, mataifa, na lugha zote, mnaamriwa kwamba, 5 wakati mtakaposikia sauti ya pembe, zumari, zeze, kinubi cha pembe tatu, kinanda, zumari-tete, na ala nyingine zote za muziki, lazima mwanguke chini na kuabudu sanamu ya dhahabu ambayo Mfalme Nebukadneza amesimamisha. 6 Yeyote ambaye hataanguka chini na kuabudu atatupwa mara moja katika tanuru lenye moto mkali.”+ 7 Basi watu wote waliposikia sauti ya pembe, zumari, zeze, kinubi cha pembe tatu, kinanda, zumari-tete, na ala nyingine zote za muziki, watu wa makabila, mataifa, na lugha zote wakaanguka chini na kuiabudu sanamu ya dhahabu ambayo Mfalme Nebukadneza alikuwa amesimamisha.
8 Wakati huo Wakaldayo fulani wakajitokeza na kuwashtaki* Wayahudi. 9 Wakamwambia Mfalme Nebukadneza: “Ee mfalme, na uishi milele. 10 Wewe, Ee mfalme, ulitoa amri kwamba kila mtu anayesikia sauti ya pembe, zumari, zeze, kinubi cha pembe tatu, kinanda, zumari-tete, na ala nyingine zote za muziki, anapaswa kuanguka chini na kuiabudu ile sanamu ya dhahabu; 11 na kwamba yeyote ambaye hataanguka chini na kuiabudu anapaswa kutupwa katika tanuru lenye moto mkali.+ 12 Lakini kuna Wayahudi fulani uliowaweka kuwa wasimamizi wa mkoa wa* Babiloni: Shadraki, Meshaki, na Abednego.+ Wanaume hawa hawajakuheshimu wewe, Ee mfalme. Hawaabudu miungu yako, na wanakataa kuabudu sanamu ya dhahabu ambayo umesimamisha.”
13 Ndipo Nebukadneza, kwa hasira kali sana, akaagiza Shadraki, Meshaki, na Abednego waletwe mbele yake. Basi wanaume hao wakaletwa mbele ya mfalme. 14 Nebukadneza akawauliza: “Shadraki, Meshaki, na Abednego, je, ni kweli kabisa kwamba hamwabudu miungu yangu+ na kwamba mnakataa kuabudu sanamu ya dhahabu ambayo nimesimamisha? 15 Basi mtakaposikia sauti ya pembe, zumari, zeze, kinubi cha pembe tatu, kinanda, zumari-tete, na ala nyingine zote za muziki, mkiwa tayari kuanguka chini na kuabudu sanamu ambayo nimeitengeneza, ni sawa. Lakini mkikataa kuabudu, mtatupwa mara moja katika tanuru lenye moto mkali. Na ni mungu gani anayeweza kuwaokoa kutoka mikononi mwangu?”+
16 Shadraki, Meshaki, na Abednego wakamjibu mfalme: “Ee Nebukadneza, hatuhitaji kukujibu kuhusiana na jambo hili. 17 Ikiwa ni lazima iwe hivyo, Mungu wetu tunayemtumikia anaweza kutuokoa kutoka katika tanuru hilo lenye moto mkali, Ee mfalme, na kutuokoa kutoka mikononi mwako.+ 18 Lakini hata asipotuokoa, Ee mfalme, ujue kwamba hatutaiabudu miungu yako wala kuabudu sanamu ya dhahabu uliyosimamisha.”+
19 Ndipo Nebukadneza akawakasirikia vikali Shadraki, Meshaki, na Abednego hivi kwamba sura yake ikabadilika * kuwaelekea, akaagiza tanuru liongezwe moto mara saba kuliko kawaida. 20 Akawaagiza wanaume fulani hodari katika jeshi lake wawafunge Shadraki, Meshaki, na Abednego na kuwatupa katika tanuru hilo lenye moto mkali.
21 Basi wanaume hao wakafungwa wakiwa na majoho yao, mavazi, kofia, na nguo zao nyingine, nao wakatupwa katika tanuru hilo lenye moto mkali. 22 Kwa sababu amri ya mfalme ilikuwa kali sana na tanuru lilikuwa na moto mkali isivyo kawaida, miali ya moto huo iliwaua wanaume waliowapeleka Shadraki, Meshaki, na Abednego. 23 Lakini wanaume hao watatu, Shadraki, Meshaki, na Abednego, wakaanguka ndani ya tanuru hilo lenye moto mkali wakiwa wamefungwa.
24 Ndipo Mfalme Nebukadneza akaogopa, akainuka haraka na kuwauliza maofisa wake wakuu: “Je, hatukuwafunga wanaume watatu na kuwatupa ndani ya moto?” Wakamjibu mfalme: “Naam, Ee mfalme.” 25 Mfalme akasema: “Tazama! Naona wanaume wanne wakitembeatembea katikati ya moto wakiwa huru, nao hawajapatwa na madhara, na yule wa nne anaonekana kama mwana wa miungu.”
26 Nebukadneza akaukaribia mlango wa lile tanuru lenye moto mkali na kusema: “Shadraki, Meshaki, na Abednego, ninyi watumishi wa Mungu Aliye Juu Zaidi,+ tokeni nje, mje hapa!” Shadraki, Meshaki, na Abednego wakatoka katikati ya moto. 27 Na maliwali, wasimamizi, magavana, na maofisa wakuu wa mfalme waliokuwa wamekusanyika mahali hapo+ wakaona kwamba moto haukuwadhuru* wanaume hao;+ hakuna unywele hata mmoja wa vichwa vyao uliokuwa umeungua, majoho yao hayakuwa yamebadilika, na miili yao haikuwa hata na harufu ya moto.
28 Ndipo Nebukadneza akatangaza hivi: “Na asifiwe Mungu wa Shadraki, Meshaki, na Abednego,+ aliyemtuma malaika wake na kuwaokoa watumishi wake. Walimtegemea yeye na kutenda kinyume cha amri ya mfalme na walikuwa tayari kufa* badala ya kumtumikia au kumwabudu mungu mwingine yeyote isipokuwa Mungu wao wenyewe.+ 29 Kwa hiyo ninaagiza kwamba watu wa kabila lolote, taifa, au lugha ambao watasema jambo lolote dhidi ya Mungu wa Shadraki, Meshaki, na Abednego, wanapaswa kukatwa vipandevipande, na nyumba zao zinapaswa kugeuzwa kuwa vyoo vya umma;* kwa maana hakuna mungu mwingine yeyote anayeweza kuokoa kama huyu.”+
30 Kisha mfalme akawapandisha vyeo* Shadraki, Meshaki, na Abednego katika mkoa wa* Babiloni.+
4 “Mimi Mfalme Nebukadneza, nawaandikia watu wa makabila yote, mataifa, na lugha zote duniani: Amani yenu na iongezeke! 2 Ninafurahi kuwatangazia ishara na maajabu ambayo Mungu Aliye Juu Zaidi amenifanyia. 3 Jinsi ishara zake zilivyo kuu, na jinsi maajabu yake yalivyo yenye nguvu! Ufalme wake ni ufalme wa milele, na utawala wake unadumu kizazi hata kizazi.+
4 “Mimi, Nebukadneza, nilikuwa nikistarehe nyumbani mwangu na kufurahia ufanisi katika jumba langu la kifalme. 5 Niliota ndoto iliyoniogopesha. Nilipokuwa nimelala kitandani mwangu, njozi na maono ya kichwa changu yalinitisha.+ 6 Basi nikaagiza wanaume wote wenye hekima wa Babiloni waletwe mbele yangu ili wanieleze maana ya ndoto hiyo.+
7 “Wakati huo makuhani wachawi, watu wanaofanya mazingaombwe, Wakaldayo,* na wanajimu+ wakaja mbele yangu. Nilipowasimulia ndoto hiyo, walishindwa kunieleza maana yake.+ 8 Mwishowe Danieli akaja mbele yangu, anayeitwa pia Belteshaza,+ jina la mungu wangu,+ na ambaye ana roho ya miungu mitakatifu,+ nami nikamwambia ndoto hiyo:
9 “‘Ee Belteshaza mkuu wa makuhani wachawi,+ ninajua vema kwamba roho ya miungu mitakatifu imo ndani yako,+ na hakuna siri yoyote iliyo ngumu sana kwako.+ Basi nieleze maono niliyoona katika ndoto yangu na maana yake.
10 “‘Katika maono ya kichwa changu nilipokuwa kitandani mwangu, niliona mti+ katikati ya dunia, nao ulikuwa mrefu kwelikweli.+ 11 Mti huo ulikua na kuimarika, na kilele chake kikafika mbinguni, nao ulionekana hadi kwenye miisho ya dunia nzima. 12 Majani yake yalipendeza, na matunda yake yalikuwa mengi, nao ulikuwa na chakula kwa ajili ya wote. Wanyama wa mwituni walitafuta kivuli chini yake, na ndege wa angani walikaa kwenye matawi yake, na viumbe wote* walipata chakula kutoka katika mti huo.
13 “‘Nilipokuwa nikitazama maono ya kichwa changu nikiwa kitandani mwangu, nilimwona mlinzi, mtakatifu, akishuka kutoka mbinguni.+ 14 Akasema hivi kwa sauti kubwa: “Ukateni na kuuangusha mti huu,+ yakateni matawi yake, yapukutisheni majani yake, na kutawanya matunda yake! Wanyama na wakimbie kutoka chini yake, na ndege kutoka kwenye matawi yake. 15 Lakini kiacheni kisiki na mizizi yake ardhini kati ya majani ya shambani, kikiwa na pingu ya chuma na ya shaba. Acheni umande wa mbinguni ukiloweshe, na acheni fungu lake liwe pamoja na wanyama, kati ya majani ya dunia.+ 16 Moyo wake na ubadilishwe usiwe wa mwanadamu, nacho kipewe moyo wa mnyama, na acheni nyakati saba+ zipite.+ 17 Hilo ni kwa agizo la walinzi,+ na ombi hilo ni kwa neno la watakatifu, ili watu walio hai wajue kwamba Aliye Juu Zaidi ni Mtawala katika ufalme wa wanadamu+ na kwamba yeye humpa ufalme huo yeyote anayetaka kumpa, naye humweka juu ya ufalme huo hata mwanadamu wa hali ya chini zaidi.”
18 “‘Hiyo ndiyo ndoto ambayo mimi, Mfalme Nebukadneza, niliota; sasa, Ee Belteshaza, nieleze maana ya ndoto hiyo, kwa maana wanaume wengine wote wenye hekima katika ufalme wangu wameshindwa kunieleza maana yake.+ Lakini wewe unaweza kufanya hivyo, kwa sababu roho ya miungu mitakatifu imo ndani yako.’
19 “Wakati huo Danieli, anayeitwa Belteshaza, akaduwaa kwa muda, na mawazo yake yakaanza kumtisha.
“Mfalme akasema, ‘Ee Belteshaza,+ usiruhusu ndoto hii na maana yake ikutishe.’
“Belteshaza akamwambia, ‘Ee bwana wangu, ndoto hii na iwahusu wale wanaokuchukia, na maana ya ndoto hiyo itimie kwa maadui wako.
20 “‘Mti ulioona ambao ulikua mpaka ukawa mkubwa na kuimarika, ambao kilele chake kilifika mbinguni na ambao ulionekana duniani pote,+ 21 uliokuwa na majani yanayopendeza, matunda mengi, na chakula kwa ajili ya wote, na ambao chini yake wanyama wa mwituni waliishi na ndege wa angani kukaa kwenye matawi yake,+ 22 ni wewe, Ee mfalme, kwa sababu umekuwa mkuu na umeimarika, na utukufu wako umeongezeka na kufika mbinguni,+ na utawala wako kwenye miisho ya dunia.+
23 “‘Wewe mfalme ulimwona mlinzi, mtakatifu,+ akishuka kutoka mbinguni, aliyekuwa akisema: “Ukateni na kuuangusha chini mti huu na kuuharibu, lakini kiacheni kisiki na mizizi yake ardhini kikiwa na pingu ya chuma na ya shaba, katikati ya majani ya shambani. Na acheni umande wa mbinguni ukiloweshe, na acheni fungu lake liwe pamoja na wanyama wa mwituni mpaka nyakati saba zipite.”+ 24 Ee mfalme, hii ndiyo maana yake; ni agizo la Aliye Juu Zaidi ambalo lazima litimie kwako bwana wangu mfalme. 25 Utafukuzwa mbali kutoka miongoni mwa wanadamu, utaishi na wanyama wa mwituni, nawe utapewa majani ule kama ng’ombe dume; na utalowa kwa umande wa mbinguni,+ na nyakati saba+ zitapita,+ mpaka utakapojua kwamba Aliye Juu Zaidi ni Mtawala katika ufalme wa wanadamu na kwamba yeye humpa ufalme huo yeyote anayetaka kumpa.+
26 “‘Lakini kwa sababu walisema kisiki cha mti huo kiachwe pamoja na mizizi yake,+ utarudishiwa tena ufalme wako baada ya kujua kwamba mbingu zinatawala. 27 Kwa hiyo, Ee mfalme, shauri langu na likubalike kwako. Geuka uziache dhambi zako kwa kutenda yaliyo sawa, na uache uovu wako kwa kuwaonyesha maskini rehema. Huenda muda wa ufanisi wako ukarefushwa.’”+
28 Hayo yote yalimpata Mfalme Nebukadneza.
29 Miezi kumi na miwili baadaye alikuwa akitembea kwenye paa la jumba lake la kifalme la Babiloni. 30 Mfalme alikuwa akisema: “Je, hii si Babiloni Kubwa ambayo nimeijenga mimi mwenyewe kuwa makao ya kifalme kwa nguvu zangu mwenyewe na uwezo wangu na kwa ajili ya utukufu wa ukuu wangu?”
31 Mfalme alipokuwa akiendelea kusema maneno hayo, sauti ikasema hivi kutoka mbinguni: “Unaambiwa hivi, Ee Mfalme Nebukadneza, ‘Ufalme umekuponyoka,+ 32 nawe unafukuzwa mbali kutoka kati ya wanadamu. Utaishi na wanyama wa mwituni, nawe utapewa majani ule kama ng’ombe dume, na nyakati saba zitapita, mpaka utakapojua kwamba Aliye Juu Zaidi ni Mtawala katika ufalme wa wanadamu na yeye humpa ufalme huo yeyote anayetaka kumpa.’”+
33 Papo hapo, maneno hayo yakatimia kwa Nebukadneza. Akafukuzwa mbali kutoka kati ya wanadamu, akaanza kula majani kama ng’ombe dume, na mwili wake ukalowa kwa umande wa mbinguni, mpaka nywele zake zikawa ndefu kama manyoya ya tai na kucha zake zikawa kama kucha za ndege.+
34 “Mwishoni mwa kipindi hicho,+ mimi, Nebukadneza, nilitazama juu mbinguni, na ufahamu wangu ukanirudia; nami nikamsifu Aliye Juu Zaidi, nikamsifu na kumtukuza Yeye anayeishi milele, kwa sababu utawala wake ni utawala wa milele na ufalme wake ni wa kizazi baada ya kizazi.+ 35 Wakaaji wote wa dunia wanaonwa kuwa si kitu, naye hufanya kulingana na mapenzi yake mwenyewe miongoni mwa jeshi la mbinguni na wakaaji wa dunia. Na hakuna yeyote anayeweza kumzuia*+ au kumuuliza, ‘Umefanya nini?’+
36 “Wakati huo ufahamu wangu ukanirudia, nami nikarudiwa na utukufu wa ufalme wangu, ukuu wangu, na fahari yangu.+ Maofisa wangu wakuu na watu mashuhuri walinitafuta kwa bidii, nami nikarudishwa kwenye ufalme wangu, na hata nikaongezewa ukuu mwingi zaidi.
37 “Sasa mimi, Nebukadneza, ninamsifu na kumkweza na kumtukuza Mfalme wa mbinguni,+ kwa sababu kazi zake zote ni kweli na njia zake ni haki,+ na kwa sababu anaweza kuwaaibisha wale wanaotembea katika kiburi.”+
5 Basi Mfalme Belshaza+ alifanya karamu kubwa kwa ajili ya wakuu wake elfu moja, naye alikuwa akinywa divai mbele yao.+ 2 Alipokuwa amelewa, Belshaza akaagiza vyombo vya dhahabu na vya fedha ambavyo Nebukadneza baba yake alikuwa amevichukua kutoka katika hekalu la Yerusalemu viletwe,+ ili avitumie kunywea divai pamoja na wakuu wake, masuria wake, na wake zake wadogo. 3 Basi wakaleta vyombo vya dhahabu vilivyochukuliwa kutoka katika hekalu la Mungu kule Yerusalemu, na mfalme pamoja na wakuu wake, masuria wake na wake zake wadogo wakavitumia kunywea divai. 4 Wakanywa divai, nao wakaisifu miungu ya dhahabu na fedha, ya shaba, chuma, miti, na mawe.
5 Wakati huohuo, vidole vya mkono wa mwanadamu vikatokea na kuanza kuandika kwenye lipu ya ukuta wa jumba la mfalme unaoelekeana na kinara cha taa, na mfalme aliweza kuona sehemu ya nyuma ya mkono huo ulipokuwa ukiandika. 6 Ndipo uso wa mfalme ukabadilika rangi* na mawazo yake yakamwogopesha, kiuno chake kikalegea+ na magoti yake yakaanza kugongana.
7 Mfalme akawaita kwa sauti kubwa watu wanaofanya mazingaombwe, Wakaldayo,* na wanajimu.+ Mfalme akawaambia wanaume hao wenye hekima wa Babiloni: “Mtu yeyote atakayesoma maandishi haya na kuniambia maana yake atavishwa mavazi ya zambarau na mkufu wa dhahabu shingoni mwake,+ naye atakuwa mtawala wa tatu katika ufalme.”+
8 Basi wanaume wote wenye hekima wa mfalme wakaja, lakini hawakuweza kusoma maandishi hayo wala kumwambia mfalme maana yake.+ 9 Kwa hiyo Mfalme Belshaza akaogopa sana na uso wake ukazidi kubadilika rangi; na wakuu wake wakapigwa na bumbuazi.+
10 Malkia aliposikia maneno ya mfalme na wakuu wake, akaingia kwenye ukumbi wa karamu. Malkia akasema: “Ee mfalme, uishi milele. Usiruhusu mawazo yako yakuogopeshe, wala usiruhusu uso wako ubadilike rangi. 11 Kuna mwanamume fulani* katika ufalme wako aliye na roho ya miungu mitakatifu. Katika siku za baba yako, mwanamume huyo alithibitika kuwa na ujuzi na ufahamu na hekima kama hekima ya miungu.+ Baba yako Mfalme Nebukadneza alimweka kuwa mkuu wa makuhani wachawi, watu wanaofanya mazingaombwe, Wakaldayo,* na wanajimu;+ hivyo ndivyo alivyofanya baba yako, Ee mfalme. 12 Kwa maana Danieli, ambaye mfalme alimwita Belteshaza,+ alikuwa na roho isiyo ya kawaida na ujuzi na ufahamu wa kueleza maana ya ndoto, kufumbua mafumbo, na kutatua matatizo magumu.*+ Basi agiza Danieli aitwe, atakwambia maana ya maandishi haya.”
13 Kwa hiyo Danieli akaletwa mbele ya mfalme. Mfalme akamuuliza Danieli: “Je, wewe ndiye Danieli, mmojawapo wa watu waliohamishwa na baba yangu mfalme kutoka Yuda?+ 14 Nimesikia kukuhusu kwamba roho ya miungu imo ndani yako+ na kwamba una ujuzi na ufahamu na hekima isiyo ya kawaida.+ 15 Sasa wanaume wenye hekima na watu wanaofanya mazingaombwe waliletwa mbele yangu ili wasome maandishi haya na kuniambia maana yake, lakini wameshindwa kuniambia maana ya ujumbe huu.+ 16 Lakini nimesikia kukuhusu kwamba unaweza kueleza maana ya mafumbo+ na kutatua matatizo magumu.* Sasa, ukifaulu kusoma maandishi haya na kuniambia maana yake, utavishwa mavazi ya zambarau na mkufu wa dhahabu shingoni mwako, nawe utakuwa mtawala wa tatu katika ufalme.”+
17 Ndipo Danieli akamwambia mfalme: “Si lazima unipe zawadi zako, unaweza kuwapa wengine zawadi hizo. Hata hivyo, nitakusomea maandishi haya na kukuambia maana yake. 18 Ee mfalme, Mungu Aliye Juu Zaidi alimpa baba yako Nebukadneza ufalme na ukuu na heshima na fahari.+ 19 Kwa sababu ya ukuu ambao Mungu alimpa, watu wa makabila yote, mataifa, na lugha walitetemeka kwa woga mbele yake.+ Yeyote ambaye mfalme alitaka kumuua, alimuua, yeyote aliyetaka kumwacha hai, alimwacha hai, yeyote aliyetaka kumkweza, alimkweza, na yeyote aliyetaka kumwaibisha, alimwaibisha.+ 20 Lakini moyo wake ulipokuwa na kiburi na roho yake kuwa ngumu hivi kwamba akatenda kwa kimbelembele,+ alishushwa chini kutoka kwenye kiti chake cha ufalme, naye akanyang’anywa heshima yake. 21 Alifukuzwa mbali kutoka kati ya wanadamu, na moyo wake ukafanywa kuwa kama wa mnyama, akaishi na punda mwitu. Alipewa majani ale kama ng’ombe dume, na mwili wake ukalowa umande wa mbinguni, mpaka alipojua kwamba Mungu Aliye Juu Zaidi ni Mtawala katika ufalme wa wanadamu na kwamba yeye humweka yeyote amtakaye juu ya ufalme huo.+
22 “Lakini wewe Belshaza, mwanawe, hujaunyenyekeza moyo wako, ingawa ulijua hayo yote. 23 Badala yake, ulijikweza mwenyewe dhidi ya Bwana wa mbinguni,+ ukawaamuru wakuletee vyombo vya nyumba yake.+ Kisha wewe pamoja na wakuu wako, masuria wako, na wake zako wadogo mkavitumia kunywea divai na kuisifu miungu ya fedha na ya dhahabu, ya shaba, chuma, miti, na mawe, miungu ambayo haioni chochote na haisikii chochote na haijui chochote.+ Lakini hujamtukuza Mungu ambaye pumzi yako na njia zako zote zimo mikononi mwake.+ 24 Kwa hiyo yeye ndiye aliyeutuma mkono huo, na maandishi haya yakaandikwa ukutani.+ 25 Na haya ndiyo maandishi yaliyoandikwa: MENE, MENE, TEKELI, na PARSINI.
26 “Hii ndiyo maana ya maneno hayo: MENE, Mungu amehesabu siku za ufalme wako na kuukomesha.+
27 “TEKELI, umepimwa katika mizani na kuonekana umepungukiwa.
28 “PERESI, ufalme wako umegawanywa wakapewa Wamedi na Waajemi.”+
29 Ndipo Belshaza akatoa amri, nao wakamvisha Danieli mavazi ya zambarau na mkufu wa dhahabu shingoni mwake; wakatangaza kwamba atakuwa mtawala wa tatu katika ufalme.+
30 Usiku huohuo Belshaza mfalme wa Wakaldayo aliuawa.+ 31 Na Dario+ Mmedi akaupokea ufalme; alikuwa na umri wa miaka 62 hivi.
6 Mfalme Dario aliona vema kuwaweka maliwali 120 kusimamia ufalme wake wote.+ 2 Juu yao kulikuwa na maofisa watatu wakuu, Danieli+ alikuwa mmoja wao; na maliwali+ walikuwa wakiwapelekea habari, ili mfalme asipate hasara. 3 Sasa, Danieli alijidhihirisha kuwa tofauti na wale maofisa wengine wakuu na maliwali, kwa maana roho isiyo ya kawaida ilikuwa ndani yake,+ na mfalme alikusudia kumkweza juu ya ufalme wote.
4 Wakati huo maofisa wakuu na maliwali walikuwa wakitafuta msingi fulani wa kumshtaki Danieli kuhusiana na mambo ya serikali,* lakini hawakuweza kupata msingi wowote wa kumshtaki wala ufisadi wowote, kwa sababu alikuwa mwenye kutegemeka, naye hakupatikana kamwe akiwa mzembe wala mfisadi. 5 Ndipo wanaume hao wakasema: “Hatutapata msingi wowote wa kumshtaki huyu Danieli, isipokuwa tutafute msingi wa kumshtaki kuhusiana na sheria ya Mungu wake.”+
6 Basi maofisa hao wakuu na maliwali wakaenda wakiwa kikundi kwa mfalme na kumwambia: “Ee Mfalme Dario, uishi milele. 7 Maofisa wote wa mfalme, wasimamizi, maliwali, maofisa wakuu wa mfalme, na magavana, wameshauriana ili mfalme atoe amri na kutangaza marufuku, kwamba kwa siku 30 mtu yeyote atakayemwomba mungu yeyote au mwanadamu isipokuwa wewe, Ee mfalme, anapaswa kutupwa ndani ya shimo la simba.+ 8 Na sasa, Ee mfalme, itoe amri hiyo na kuitia sahihi,+ ili isiweze kubadilishwa kulingana na sheria ya Wamedi na Waajemi, ambayo haiwezi kufutwa.”+
9 Kwa hiyo Mfalme Dario akatia sahihi amri hiyo na marufuku hayo.
10 Lakini mara tu Danieli alipojua kwamba amri hiyo imetiwa sahihi alienda nyumbani kwake, na madirisha ya chumba chake kilichokuwa darini yalikuwa yamefunguliwa kuelekea Yerusalemu.+ Na mara tatu kwa siku alipiga magoti na kusali na kumsifu Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya kwa ukawaida kabla ya mambo hayo. 11 Wakati huo wanaume hao wakaingia kwa kishindo na kumkuta Danieli akimwomba na kumsihi Mungu wake apate kibali mbele zake.
12 Kwa hiyo wakaenda kwa mfalme na kumkumbusha kuhusu marufuku aliyotangaza: “Je, hukutia sahihi marufuku ukisema kwamba kwa siku 30 mtu yeyote atakayemwomba mungu yeyote au mwanadamu yeyote isipokuwa wewe, Ee mfalme, anapaswa kutupwa ndani ya shimo la simba?” Mfalme akasema: “Hivyo ndivyo ilivyo kulingana na sheria ya Wamedi na Waajemi, isiyoweza kufutwa.”+ 13 Mara moja wakamwambia mfalme: “Danieli, mmoja wa watu waliohamishwa kutoka Yuda+ hajakuheshimu wewe, Ee mfalme, wala marufuku uliyotia sahihi, badala yake anasali mara tatu kwa siku.”+ 14 Mara tu mfalme aliposikia hivyo, alihuzunika sana, akajaribu kutafuta njia ya kumwokoa Danieli; alifanya kila jitihada ya kumwokoa mpaka jua likatua. 15 Mwishowe wanaume hao wakaenda mbele ya mfalme wakiwa kikundi na kumwambia: “Ee mfalme, zingatia kwamba sheria ya Wamedi na Waajemi inasema kwamba marufuku yoyote au amri yoyote iliyowekwa na mfalme haiwezi kubadilishwa.”+
16 Basi mfalme akatoa agizo, nao wakamleta Danieli na kumtupa ndani ya shimo la simba.+ Mfalme akamwambia Danieli: “Mungu wako unayemtumikia daima, atakuokoa.” 17 Kisha jiwe likaletwa na kuwekwa kwenye mwingilio* wa shimo hilo, naye mfalme akalitia muhuri kwa pete yake ya muhuri na kwa pete ya muhuri ya wakuu wake ili uamuzi kumhusu Danieli usibadilishwe hata kidogo.
18 Kisha mfalme akaenda kwenye jumba lake la kifalme. Akafunga usiku kucha na kukataa kutumbuizwa kwa njia yoyote,* naye akashindwa kulala usingizi.* 19 Hatimaye, alfajiri na mapema, mfalme aliondoka na kwenda haraka kwenye lile shimo la simba. 20 Alipokaribia shimo hilo, akamwita Danieli kwa sauti ya huzuni. Mfalme akamuuliza Danieli: “Ee Danieli, mtumishi wa Mungu aliye hai, je, Mungu wako unayemtumikia daima ameweza kukuokoa kutoka kwa simba hao?” 21 Mara moja Danieli akamjibu mfalme: “Ee mfalme, uishi milele. 22 Mungu wangu alimtuma malaika wake akafunga vinywa vya simba,+ nao hawajanidhuru,+ kwa sababu sikupatikana na hatia mbele zake; wala sijakutendea jambo lolote baya, Ee mfalme.”
23 Mfalme akafurahi sana, akaamuru Danieli atolewe ndani ya lile shimo. Danieli alipotolewa shimoni, hakuwa amepatwa na madhara yoyote, kwa sababu alikuwa amemtumaini Mungu wake.+
24 Kisha mfalme akatoa agizo, na wanaume waliokuwa wamemshtaki* Danieli wakaletwa, nao wakatupwa ndani ya lile shimo la simba, pamoja na wake zao na watoto wao. Kabla hawajafika chini shimoni, simba waliwashinda nguvu na kuvunjavunja mifupa yao yote.+
25 Kisha Mfalme Dario akawaandikia watu wa makabila yote, mataifa, na lugha wanaokaa katika dunia yote:+ “Muwe na amani tele! 26 Ninatoa agizo kwamba katika kila eneo la ufalme wangu, watu wanapaswa kutetemeka kwa woga mbele za Mungu wa Danieli.+ Kwa maana yeye ndiye Mungu aliye hai naye huishi milele. Ufalme wake hautaangamizwa kamwe, na utawala wake ni wa* milele.+ 27 Yeye huokoa,+ naye hufanya ishara na maajabu mbinguni na duniani,+ kwa sababu alimwokoa Danieli kutoka katika makucha ya simba.”
28 Basi Danieli huyo akafanikiwa katika ufalme wa Dario+ na katika ufalme wa Koreshi Mwajemi.+
7 Katika mwaka wa kwanza wa utawala wa Mfalme Belshaza+ wa Babiloni, Danieli aliota ndoto na kuona maono akiwa amelala kitandani mwake.+ Kisha akaandika ndoto hiyo;+ akaandika masimulizi kamili ya mambo hayo. 2 Danieli akasema:
“Nilikuwa nikitazama katika maono yangu wakati wa usiku, na tazama! pepo nne za mbingu, zilikuwa zikivuruga bahari kubwa sana.+ 3 Na wanyama wanne+ wakubwa sana wakatoka katika bahari hiyo, kila mmoja alikuwa tofauti na wenzake.
4 “Wa kwanza alikuwa kama simba,+ naye alikuwa na mabawa ya tai.+ Nikatazama mpaka mabawa yake yakang’olewa, akainuliwa kutoka duniani na kusimamishwa kwa miguu miwili kama mwanadamu, naye akapewa moyo wa mwanadamu.
5 “Na tazama! mnyama mwingine, wa pili, kama dubu.+ Aliinuliwa upande mmoja, na mbavu tatu zilikuwa kinywani mwake kati ya meno yake; naye akaambiwa, ‘Simama, kula nyama nyingi.’+
6 “Baada ya hayo nikaendelea kuangalia, na tazama! mnyama mwingine, kama chui,+ lakini mgongoni mwake alikuwa na mabawa manne kama ya ndege. Na mnyama huyo alikuwa na vichwa vinne,+ naye alipewa mamlaka ya kutawala.
7 “Baada ya hayo nikaendelea kutazama katika maono ya usiku, nikaona mnyama wa nne, mwenye kuogopesha na mwenye kutisha, na mwenye nguvu isivyo kawaida, naye alikuwa na meno makubwa ya chuma. Alikuwa akinyafua na kuvunjavunja, na kilichobaki alikikanyaga-kanyaga chini kwa miguu yake.+ Alikuwa tofauti na wanyama wote waliomtangulia, naye alikuwa na pembe kumi. 8 Nilipokuwa nikiangalia pembe hizo, tazama! pembe nyingine, ndogo,+ ikajitokeza miongoni mwa pembe hizo, na pembe tatu kati ya zile za kwanza zikang’olewa mbele yake. Na, tazama! pembe hiyo ilikuwa na macho kama ya mwanadamu, na ilikuwa na kinywa kinachozungumza kwa kiburi.*+
9 “Nikaendelea kutazama mpaka viti vya ufalme vikawekwa na Mzee wa Siku+ akaketi.+ Mavazi yake yalikuwa meupe kama theluji,+ na nywele za kichwa chake zilikuwa kama sufu safi. Kiti chake cha ufalme kilikuwa miali ya moto; magurudumu yake yalikuwa moto unaowaka.+ 10 Mto wa moto ulikuwa ukitiririka kutoka mbele zake.+ Elfu kwa maelfu waliendelea kumhudumia, na elfu kumi mara elfu kumi walisimama mbele zake.+ Mahakama+ ikaketi, na vitabu vikafunguliwa.
11 “Nikaendelea kutazama wakati huo kwa sababu ya mvumo wa maneno ya kiburi* yaliyokuwa yakisemwa na pembe hiyo;+ nilitazama mpaka mnyama huyo alipouawa na mwili wake ukaharibiwa na kutolewa ili uchomwe moto. 12 Lakini wale wanyama wengine+ walinyang’anywa tawala zao, na maisha yao yakarefushwa kwa wakati mmoja na majira.
13 “Nikaendelea kuangalia katika maono ya usiku, na tazama! mtu fulani kama mwana wa binadamu+ alikuwa akija na mawingu ya mbinguni; naye akaja mbele za Mzee wa Siku,+ nao wakamleta karibu Naye. 14 Naye akapewa utawala,+ heshima,+ na ufalme, ili watu wa makabila, mataifa, na lugha zote wamtumikie.+ Utawala wake ni utawala wa milele ambao hautapitilia mbali, na ufalme wake hautaangamizwa.+
15 “Basi, mimi Danieli, roho yangu ilifadhaika kwa sababu maono ya kichwa changu yaliniogopesha.+ 16 Nikamkaribia mmoja wa wale waliokuwa wamesimama pale ili nimuulize maana halisi ya mambo hayo. Basi akanijibu na kunieleza maana ya mambo hayo.
17 “‘Wanyama hawa wakubwa, wanne,+ ni wafalme wanne ambao watasimama kutoka duniani.+ 18 Lakini watakatifu wa Aliye Mkuu Zaidi+ watapokea ule ufalme,+ nao wataumiliki ufalme huo+ milele, naam, milele na milele.’
19 “Kisha nikataka kujua mengi zaidi kuhusu yule mnyama wa nne, ambaye alikuwa tofauti na wale wengine; alikuwa mwenye kuogopesha isivyo kawaida; alikuwa na meno ya chuma na makucha ya shaba, naye alikuwa akinyafua na kuvunjavunja, na kukanyaga-kanyaga chini kwa miguu yake kilichobaki;+ 20 na pia kuhusu zile pembe kumi+ zilizokuwa kichwani mwake, na ile pembe nyingine iliyojitokeza na ambayo mbele yake pembe tatu zilianguka,+ pembe iliyokuwa na macho na kinywa kilichozungumza kwa kiburi* na ambayo umbo lake lilikuwa kubwa kuliko umbo la zile pembe nyingine.
21 “Nikaendelea kutazama pembe hiyo ilipokuwa ikiwapiga vita watakatifu, nayo ilikuwa ikiwashinda,+ 22 mpaka Mzee wa Siku+ alipokuja na kuhukumu kwa faida ya watakatifu wa Aliye Mkuu Zaidi,+ na wakati uliowekwa ukafika wa watakatifu kuumiliki ufalme.+
23 “Alisema hivi: ‘Kuhusu yule mnyama wa nne, kuna ufalme wa nne utakaotokea duniani. Utakuwa tofauti na falme nyingine zote, nao utainyafua dunia yote na kuikanyaga-kanyaga chini na kuivunjavunja.+ 24 Kuhusu zile pembe kumi, wafalme kumi watainuka kutoka katika ufalme huo; na bado kuna mwingine atakayeinuka baada yao, atakuwa tofauti na wale wa kwanza, naye atawaaibisha wafalme watatu.+ 25 Atasema maneno dhidi ya Aliye Juu Zaidi,+ naye ataendelea kuwanyanyasa watakatifu wa Aliye Mkuu Zaidi. Atakusudia kubadili nyakati na sheria, nao watatiwa mikononi mwake kwa wakati, nyakati, na nusu wakati.*+ 26 Lakini ile Mahakama ikaketi, nao wakamnyang’anya utawala wake, ili wamwangamize na kumharibu kabisa.+
27 “‘Na ufalme na utawala na utukufu wa falme chini ya mbingu zote ulikabidhiwa watu ambao ni watakatifu wa Aliye Mkuu Zaidi.+ Ufalme wao ni ufalme wa milele,+ na tawala zote zitawatumikia na kuwatii wao.’
28 “Huu ndio mwisho wa jambo hilo. Basi mimi, Danieli, mawazo yangu yaliniogopesha sana, hivi kwamba uso wangu ukabadilika* rangi; lakini niliweka jambo hilo katika moyo wangu mwenyewe.”
8 Katika mwaka wa tatu wa utawala wa Mfalme Belshaza,+ mimi, Danieli, niliona maono, baada ya yale niliyoona mwanzoni.+ 2 Niliona maono hayo, na nilipokuwa nikiyaona nilikuwa katika ngome ya* Shushani,*+ iliyo katika mkoa wa* Elamu;+ niliona maono hayo, nami nilikuwa kando ya mfereji wa maji wa Ulai. 3 Nilipoinua macho yangu, tazama! kulikuwa na kondoo dume+ aliyesimama mbele ya mfereji huo wa maji, naye alikuwa na pembe mbili.+ Pembe hizo mbili zilikuwa ndefu, lakini moja ilikuwa ndefu kuliko nyingine, na pembe hiyo ndefu ilitokea baadaye.+ 4 Nikamwona huyo kondoo dume akisonga mbele kwa nguvu kuelekea magharibi, kaskazini, na kusini, na hakuna mnyama yeyote wa mwituni aliyeweza kusimama mbele yake, wala hakukuwa na yeyote aliyeweza kuokoa kutoka katika nguvu zake.*+ Alifanya apendavyo na kujikweza.
5 Nilipokuwa nikiendelea kuangalia, tazama! kulikuwa na mbuzi dume+ aliyekuwa akija kutoka magharibi* akivuka dunia yote bila kugusa ardhi. Na mbuzi huyo alikuwa na pembe iliyoonekana waziwazi kati ya macho yake.+ 6 Alikuwa akija kumwelekea yule kondoo dume mwenye pembe mbili ambaye nilimwona amesimama mbele ya ule mfereji wa maji; alikuwa akikimbia kumwelekea kwa ghadhabu kubwa.
7 Nikamwona akimkaribia yule kondoo dume, naye alikuwa amejawa na uchungu mwingi kumwelekea. Akampiga na kumwangusha chini huyo kondoo dume na kuzivunja pembe zake mbili, na kondoo dume huyo hakuwa na nguvu za kustahimili. Basi akamwangusha ardhini kondoo dume huyo na kumkanyaga-kanyaga, na hakukuwa na yeyote wa kumwokoa kutoka katika nguvu zake.*
8 Kisha huyo mbuzi dume akajikweza kupita kiasi, lakini mara tu alipokuwa na nguvu, ile pembe kubwa ikavunjika; kisha mahali pake zikatokea pembe nne zilizokuwa zikionekana waziwazi, kuelekea zile pepo nne za mbingu.+
9 Pembe nyingine ndogo ilitokea katika mojawapo ya pembe hizo, nayo ikakua ikawa kubwa sana kuelekea kusini na kuelekea mashariki* na kuelekea lile Pambo.*+ 10 Ikawa kubwa sana hivi kwamba ikalifikia jeshi la mbinguni, nayo ikasababisha sehemu ya jeshi hilo na baadhi ya nyota zianguke duniani, nayo ikazikanyaga-kanyaga. 11 Ikajikweza hata dhidi ya Mkuu wa jeshi hilo, na ile dhabihu inayotolewa daima ikaondolewa* kutoka kwake, na mahali pake patakatifu palipo imara pakatupwa chini.+ 12 Na kwa sababu ya uasi, jeshi likatiwa mikononi mwa pembe hiyo, pamoja na ile dhabihu inayotolewa daima,* nayo iliendelea kuutupa ukweli duniani, ikatenda na kufanikiwa.
13 Nami nikamsikia mtakatifu akizungumza, na mtakatifu mwingine akamuuliza mtakatifu aliyekuwa akizungumza: “Maono ya dhabihu inayotolewa daima* na ya uasi unaosababisha ukiwa yataendelea kwa muda gani+ kufanya mahali patakatifu na lile jeshi kuwa vitu vya kukanyagwa-kanyagwa?” 14 Basi akaniambia: “Kwa muda wa jioni na asubuhi 2,300; na hakika mahali patakatifu patarudishwa katika hali yake inayofaa.”
15 Mimi, Danieli, nilipokuwa nikiona maono hayo na kujaribu kuyaelewa, kwa ghafla nikamwona mtu fulani aliyeonekana kama mwanamume amesimama mbele yangu. 16 Kisha nikasikia sauti ya mwanamume katikati ya mfereji wa Ulai,+ akaita kwa sauti kubwa: “Gabrieli,+ mweleweshe mtu huyo mambo aliyoona.”+ 17 Kwa hiyo akakaribia mahali nilipokuwa nimesimama, lakini alipokuja niliogopa sana hivi kwamba nikaanguka chini kifudifudi. Akaniambia: “Elewa, Ee mwana wa binadamu, kwamba maono hayo ni ya wakati wa mwisho.”+ 18 Lakini alipokuwa akizungumza nami, nilishikwa na usingizi mzito huku nikiwa nimeanguka chini kifudifudi. Basi akanigusa na kunisimamisha mahali nilipokuwa nimesimama mwanzoni.+ 19 Kisha akasema: “Ninakujulisha yatakayotokea katika sehemu ya mwisho ya shutuma, kwa sababu maono hayo yanahusu wakati uliowekwa wa mwisho.+
20 “Yule kondoo dume mwenye pembe mbili uliyemwona anafananisha wafalme wa Umedi na Uajemi.+ 21 Yule mbuzi dume mwenye manyoya anafananisha mfalme wa Ugiriki;+ na ile pembe kubwa iliyokuwa kati ya macho yake, inafananisha mfalme wa kwanza.+ 22 Kuhusu ile pembe iliyovunjika, kisha pembe nne zikatokea badala yake,+ kuna falme nne kutoka katika taifa lake zitakazosimama, lakini hazitakuwa na nguvu kama zake.
23 “Na katika kipindi cha mwisho cha ufalme wao, waasi watakapofikia kilele cha kutenda maovu, mfalme mwenye uso mkali anayeelewa mafumbo* atatokea. 24 Atakuwa na nguvu nyingi, lakini si kwa uwezo wake mwenyewe. Ataleta uharibifu kwa njia isiyo ya kawaida,* naye atafanikiwa katika kila analotenda. Atawaangamiza wenye nguvu, na pia watu watakatifu.+ 25 Na kwa ujanja wake atatumia udanganyifu kufanikiwa; na katika moyo wake atajikweza; na atawaangamiza watu wengi wakati wa usalama.* Hata atasimama dhidi ya Mkuu wa wakuu, lakini atavunjwa si kwa mkono wa mwanadamu.
26 “Mambo yaliyosemwa katika maono kuhusu jioni na asubuhi hizo ni ya kweli, lakini ni lazima uyaweke siri maono hayo, kwa sababu yanahusu kipindi cha siku nyingi kutoka sasa.”*+
27 Basi mimi, Danieli, nilichoka sana nikawa mgonjwa kwa siku kadhaa.+ Kisha nikaamka na kufanya kazi ya mfalme;+ lakini mambo niliyokuwa nimeona yalifanya nife ganzi, na hakuna yeyote aliyeweza kuelewa maono hayo.+
9 Katika mwaka wa kwanza wa utawala wa Dario+ mwana wa Ahasuero—mzao wa Wamedi aliyekuwa amewekwa kuwa mfalme wa ufalme wa Wakaldayo+— 2 katika mwaka wa kwanza wa utawala wake, mimi, Danieli, nilitambua kutokana na vitabu* idadi ya miaka iliyokuwa imetajwa katika neno la Yehova kwa nabii Yeremia ili kutimiza ukiwa wa Yerusalemu,+ yaani, miaka 70.+ 3 Basi nikageuza uso wangu kumwelekea Yehova Mungu wa kweli, nikimsihi katika sala, pamoja na kufunga+ na kuvaa nguo za magunia na kujimwagia majivu. 4 Nilisali kwa Yehova Mungu wangu, nikaungama na kusema:
“Ee Yehova Mungu wa kweli, Mungu mkuu na Mwenye kuogopesha, unayeshika agano lako na kuwatendea kwa upendo mshikamanifu+ wale wanaokupenda na kushika amri zako,+ 5 tumetenda dhambi na tumekosea na tumetenda uovu na kuasi;+ nasi tumegeuka na kuacha amri zako na sheria* zako. 6 Hatujawasikiliza watumishi wako manabii,+ ambao kwa jina lako walizungumza na wafalme wetu, wakuu wetu, mababu zetu, na watu wote nchini. 7 Ee Yehova, uadilifu ni wako, lakini aibu ni yetu kama ilivyo leo, sisi watu wa Yuda, wakaaji wa Yerusalemu, na Waisraeli wote, wale walio karibu na walio mbali, katika nchi zote ambazo uliwatawanya kwa sababu hawakutenda kwa uaminifu kukuelekea.+
8 “Ee Yehova, aibu ni yetu, wafalme wetu, wakuu wetu, na mababu zetu, kwa sababu tumekutendea dhambi. 9 Rehema na msamaha ni zako Yehova Mungu wetu,+ kwa maana tumekuasi.+ 10 Hatujaitii sauti yako Yehova Mungu wetu kwa kufuata sheria zako ulizotupatia kupitia watumishi wako manabii.+ 11 Waisraeli wote wamekiuka Sheria yako na kukuacha kwa kutotii sauti yako, hivi kwamba ukatumwagia laana na kiapo kilichoandikwa katika Sheria ya Musa mtumishi wa Mungu wa kweli,+ kwa maana tumekutendea Wewe dhambi. 12 Umetimiza maneno uliyosema dhidi yetu+ na dhidi ya watawala wetu waliotutawala,* kwa kutuletea msiba mkubwa; hakuna jambo lililowahi kufanywa chini ya mbingu zote kama jambo lililofanywa Yerusalemu.+ 13 Kama tu ilivyoandikwa katika Sheria ya Musa, msiba huu wote umetujia,+ lakini hatujakuomba kibali* Yehova Mungu wetu kwa kuacha uovu wetu+ na kwa kuonyesha ufahamu katika ukweli* wako.
14 “Basi Yehova ukakaa macho na kutuletea msiba, kwa maana wewe Yehova Mungu wetu ni mwadilifu katika kazi zote ambazo umefanya; hata hivyo sisi hatujaitii sauti yako.+
15 “Sasa, Ee Yehova Mungu wetu, Wewe uliyewatoa watu wako nchini Misri kwa mkono wenye nguvu,+ na kujijengea jina hadi leo hii,+ tumefanya dhambi na kutenda uovu. 16 Ee Yehova, kulingana na matendo yako yote ya uadilifu,+ tafadhali, iondoe hasira na ghadhabu yako kutoka katika jiji lako Yerusalemu, mlima wako mtakatifu; kwa maana dhambi zetu na makosa ya mababu zetu yamefanya Yerusalemu na watu wako wawe kitu cha kushutumiwa na watu wote wanaotuzunguka.+ 17 Na sasa sikiliza, Ee Mungu wetu, sala yangu mimi mtumishi wako na maombi yangu, na ufanye uso wako uangaze juu ya mahali pako patakatifu+ palipo ukiwa,+ kwa ajili yako mwenyewe, Ee Yehova. 18 Tega sikio lako, Ee Mungu wangu, usikie! Fungua macho yako uone hali yetu ya ukiwa na jiji ambalo limeitwa kwa jina lako; kwa maana hatukuombi kwa sababu ya matendo yetu ya uadilifu bali kwa sababu ya rehema yako kuu.+ 19 Ee Yehova, sikia. Ee Yehova, samehe.+ Ee Yehova, sikiliza kwa makini na uchukue hatua. Usikawie, kwa ajili yako mwenyewe, Ee Mungu wangu, kwa maana jiji lako na watu wako wameitwa kwa jina lako mwenyewe.”+
20 Nilipokuwa bado nikiongea na kusali na kuungama dhambi yangu na dhambi ya watu wangu Waisraeli na kuomba kibali mbele za Yehova Mungu wangu kuhusu mlima mtakatifu wa Mungu wangu,+ 21 naam, nilipokuwa bado nikisali, mwanamume Gabrieli,+ niliyekuwa nimemwona awali katika maono,+ alinijia nilipokuwa nimechoka kwelikweli karibu wakati ambao zawadi ya jioni hutolewa. 22 Naye akanipa uelewaji akisema:
“Ee Danieli, sasa nimekuja kukupa ufahamu na uelewaji. 23 Ulipoanza kusali jibu lilitolewa, nami nimekuja kukujulisha jibu hilo, kwa sababu wewe ni mtu mwenye thamani sana.*+ Basi zingatia ujumbe huu na kuelewa maono haya.
24 “Kuna majuma 70* ambayo yameamuliwa kwa ajili ya watu wako na kwa ajili ya jiji lako takatifu,+ ili kukomesha uasi, kumaliza kabisa dhambi,+ kufunika makosa,+ kuleta uadilifu wa milele,+ kutia muhuri maono na unabii,*+ na kutia mafuta Patakatifu pa Patakatifu.* 25 Unapaswa kujua na kuelewa kwamba tangu kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu+ mpaka atakapotokea Masihi*+ aliye Kiongozi,+ kutakuwa na majuma 7, na pia majuma 62.+ Yerusalemu litarudishwa na kujengwa upya, pamoja na uwanja wa jiji na handaki, lakini katika nyakati za taabu.
26 “Na baada ya hayo majuma 62, Masihi atauawa,*+ hatabaki na chochote.+
“Na watu wa kiongozi anayekuja wataliharibu jiji na mahali patakatifu.+ Na mwisho wake utakuwa kwa mafuriko. Na mpaka ule mwisho kutakuwa na vita; kilichoamuliwa ni ukiwa.+
27 “Naye atalitendesha agano kwa ajili ya wengi kwa juma moja; na katika nusu ya juma hilo atakomesha dhabihu na toleo la zawadi.+
“Na juu ya bawa la vitu vyenye kuchukiza sana kutakuwa na yule anayesababisha ukiwa;+ na mpaka wakati wa maangamizi, kilichoamuliwa kitamwagwa pia juu ya yule anayekaa ukiwa.”
10 Katika mwaka wa tatu wa utawala wa Koreshi+ mfalme wa Uajemi, Danieli ambaye pia aliitwa Belteshaza+ alipewa ufunuo; na ujumbe wake ulikuwa wa kweli, nao ulihusu pambano kubwa. Naye alielewa ujumbe huo na kupewa uelewaji kuhusu mambo aliyokuwa ameona.
2 Siku hizo, mimi, Danieli, nilikuwa nikiomboleza+ kwa majuma matatu kamili. 3 Sikula kamwe chakula kizuri, sikula nyama wala kunywa divai, nami sikujipaka kamwe mafuta kwa majuma matatu kamili. 4 Katika siku ya 24 ya mwezi wa kwanza, nilipokuwa kwenye ukingo wa ule mto mkubwa, Mto Tigri,*+ 5 niliinua macho yangu nikamwona mwanamume aliyevaa mavazi ya kitani,+ na kiunoni mwake alikuwa na mshipi wa dhahabu kutoka Ufazi. 6 Mwili wake ulikuwa kama krisolito,+ uso wake ulionekana kama radi, macho yake yalikuwa kama mienge inayowaka moto, mikono yake na miguu yake ilionekana kama shaba iliyong’arishwa,+ na mvumo wa maneno yake ulikuwa kama mvumo wa umati wa watu. 7 Ni mimi Danieli, peke yangu, niliyeona maono hayo; wanaume waliokuwa pamoja nami hawakuyaona.+ Hata hivyo, walishikwa na hofu kubwa, wakakimbia na kujificha.
8 Kisha nikabaki peke yangu, na nilipoona maono hayo makubwa nguvu ziliniishia na sura yangu ya heshima ikatoweka, nikapoteza nguvu zote.+ 9 Kisha nikasikia sauti yake akizungumza; lakini nilipomsikia akizungumza, nikalala kifudifudi ardhini na kushikwa na usingizi mzito.+ 10 Lakini mkono ukanigusa,+ ukanitikisa ili niinuke kwa mikono na magoti yangu. 11 Kisha akaniambia:
“Ee Danieli, wewe mtu mwenye thamani sana,*+ sikiliza kwa makini maneno ninayotaka kukwambia. Sasa simama mahali ulipo, kwa maana nimetumwa kwako.”
Aliponiambia maneno hayo, nikasimama nikitetemeka.
12 Kisha akaniambia: “Usiogope,+ Ee Danieli. Maneno yako yamesikiwa tangu siku ya kwanza ulipoukaza moyo wako kupata uelewaji na kujinyenyekeza mbele za Mungu wako, nami nimekuja kwa sababu ya maneno yako.+ 13 Lakini mkuu+ wa ufalme wa Uajemi alinipinga kwa siku 21. Lakini Mikaeli,*+ mmoja wa wakuu wenye vyeo vya juu zaidi,* akaja kunisaidia; nami nikabaki huko kando ya wafalme wa Uajemi. 14 Nimekuja kukuelewesha mambo yatakayowapata watu wako katika kipindi cha mwisho cha zile siku,+ kwa maana ni maono yanayohusu siku zijazo.”+
15 Sasa aliponiambia maneno hayo, niliuinamisha uso wangu chini nikashindwa kuongea. 16 Ndipo mmoja aliyeonekana kama mwanadamu akaigusa midomo yangu,+ nami nikafungua kinywa changu na kumwambia yule aliyesimama mbele yangu: “Bwana wangu ninaogopa kwa sababu ya maono hayo, nami sina nguvu.+ 17 Sasa bwana wangu, mimi mtumishi wako, ninawezaje kuzungumza nawe bwana wangu?+ Kwa maana sasa sina nguvu, na pumzi imeniishia.”+
18 Yule aliyeonekana kama mwanadamu akanigusa tena na kunitia nguvu.+ 19 Kisha akasema: “Usiogope,+ Ee mtu mwenye thamani sana.*+ Uwe na amani.+ Uwe na nguvu, naam, uwe na nguvu.” Alipokuwa akizungumza nami nilitiwa nguvu na kusema: “Bwana wangu, sema, kwa maana umenitia nguvu.”
20 Ndipo akasema: “Je, unajua kwa nini nimekuja? Sasa nitarudi kupigana na mkuu wa Uajemi.+ Nitakapoondoka, mkuu wa Ugiriki atakuja. 21 Hata hivyo, nitakwambia mambo yaliyoandikwa katika kitabu cha kweli. Hakuna yeyote anayeniunga mkono kwa uthabiti katika mambo haya isipokuwa Mikaeli,+ mkuu wako.+
11 “Mimi, katika mwaka wa kwanza wa utawala wa Dario+ Mmedi, nilisimama ili kumtia nguvu na kumwimarisha.* 2 Nitakayokwambia sasa ndiyo kweli:
“Tazama! Wafalme watatu zaidi watasimama* kwa ajili ya Uajemi, na wa nne atajikusanyia utajiri mwingi zaidi kuliko wengine wote. Na atakapokuwa na nguvu kupitia utajiri wake, atachochea kila kitu dhidi ya ufalme wa Ugiriki.+
3 “Na mfalme mwenye nguvu atasimama na kutawala kwa mamlaka kubwa sana+ na kufanya apendavyo. 4 Na atakapokuwa amesimama, ufalme wake utavunjwa na kugawanywa kuelekea pepo nne za mbinguni,+ lakini si kwa wazao wake* na si kwa mamlaka aliyotawala nayo; kwa maana ufalme wake utang’olewa na kuchukuliwa na wengine zaidi ya hao.
5 “Na mfalme wa kusini atakuwa na nguvu, yaani, mmoja wa wakuu wake; lakini kuna mmoja atakayemshinda na kutawala kwa mamlaka kubwa sana, kubwa kuliko mamlaka yake.
6 “Baada ya miaka kadhaa wataungana, na binti ya mfalme wa kusini atakuja kwa mfalme wa kaskazini ili kufanya makubaliano. Lakini nguvu za mkono wa binti huyo hazitadumu; na mfalme huyo hatasimama, wala mkono wake; na binti huyo atatiwa mikononi mwa wengine, yeye pamoja na wale wanaomleta, na yule aliyemzaa, na yule atakayemtia nguvu nyakati hizo. 7 Na mmoja kutoka katika chipukizi la mizizi yake atasimama katika cheo cha mfalme huyo, na mfalme huyo atalijia jeshi na kushambulia ngome ya mfalme wa kaskazini naye atachukua hatua dhidi yao na kushinda. 8 Mfalme huyo atakuja Misri pamoja na miungu yao, sanamu zao za chuma,* na vitu vyao vinavyotamanika* vya fedha na vya dhahabu, pamoja na mateka. Kwa miaka kadhaa hatamshambulia mfalme wa kaskazini, 9 ambaye ataushambulia ufalme wa mfalme wa kusini, lakini atarudi katika nchi yake mwenyewe.
10 “Na wanawe watajitayarisha kwa ajili ya vita na kukusanya jeshi kubwa sana. Naye hakika atasonga mbele na kupita kama mafuriko. Lakini atarudi, naye atapigana vita mpaka kwenye ngome yake.
11 “Na mfalme wa kusini atakasirika, naye atatoka na kwenda kupigana naye, yaani, na mfalme wa kaskazini, ambaye atakusanya umati mkubwa wa watu, lakini umati huo utatiwa mikononi mwa mfalme huyo.* 12 Na umati huo utachukuliwa. Moyo wake utajikweza, naye atasababisha makumi ya maelfu waanguke; lakini hatatumia nafasi aliyopata ya ushindi.
13 “Na mfalme wa kaskazini atarudi na kukusanya umati mkubwa zaidi kuliko ule wa kwanza; na mwishoni mwa zile nyakati, baada ya miaka kadhaa, kwa hakika atakuja na jeshi kubwa na mali nyingi. 14 Nyakati hizo wengi watampinga mfalme wa kusini.
“Na watu wakatili* miongoni mwa watu wako watashawishiwa kujaribu kutimiza maono; lakini watajikwaa.
15 “Na mfalme wa kaskazini atakuja na kujenga boma la kuzingira na kuteka jiji lenye ngome. Na majeshi ya kusini hayatasimama,* wala wanaume wake mashujaa; nao hawatakuwa na nguvu za kusimama. 16 Yule anayekuja kupigana naye atafanya apendavyo, na hakuna yeyote atakayesimama mbele yake. Atasimama katika nchi ya lile Pambo,*+ na uwezo wa kuangamiza utakuwa mikononi mwake. 17 Naye ataazimia kabisa* kuja na nguvu kamili za ufalme wake, atafanya makubaliano pamoja na mfalme huyo; naye atatenda kwa mafanikio. Na kumhusu yule binti wa wanawake, mfalme huyo atapewa ruhusa ya kumwangamiza. Na binti huyo hatasimama, wala hataendelea kuwa wake. 18 Mfalme huyo ataugeuza uso wake na kurudi kwenye nchi za pwani, naye atateka maeneo mengi. Na kamanda fulani atakomesha kwa faida yake mwenyewe ufidhuli kutoka kwa mfalme huyo, hivi kwamba ufidhuli huo hautakuwepo. Ataufanya umrudie mfalme huyo. 19 Kisha* ataugeuza uso wake kurudi kwenye ngome za nchi yake mwenyewe, naye atajikwaa na kuanguka, na hatapatikana.
20 “Na katika cheo chake atasimama mtu anayemfanya mtozaji* apite katika ufalme wenye fahari, lakini katika siku chache atavunjwa, ingawa si kwa hasira wala vitani.
21 “Na katika cheo chake atasimama mtu anayedharauliwa,* nao hawatampa fahari ya ufalme huo; naye atakuja wakati wa usalama* na kuchukua ufalme kwa ujanja.* 22 Na majeshi yaliyo kama mafuriko yatafagiliwa* mbali kwa sababu yake, nayo yataangamizwa; kama itakavyokuwa kwa Kiongozi+ wa lile agano.+ 23 Na kwa sababu ya muungano waliofanya naye, ataendeleza udanganyifu na kuinuka na kuwa mwenye nguvu kupitia taifa dogo. 24 Wakati wa usalama,* atavamia maeneo ya mkoa* yenye utajiri mwingi zaidi* na kufanya mambo ambayo baba zake na mababu zake hawakufanya. Atawagawia watu wake vitu alivyopora na nyara na mali; naye atapanga njama zake dhidi ya mahali penye ngome, lakini kwa muda tu.
25 “Akiwa na jeshi kubwa, atakusanya nguvu zake na moyo wake dhidi ya mfalme wa kusini, naye mfalme wa kusini atajitayarisha kwa ajili ya vita hivyo akiwa na jeshi kubwa kupita kiasi, tena lenye nguvu. Naye hatasimama, kwa sababu watapanga njama dhidi yake. 26 Na wale wanaokula vyakula vyake bora watasababisha aanguke.
“Na jeshi lake litafagiliwa mbali, na wengi watauawa.
27 “Kuhusu wafalme hawa wawili, moyo wao utakuwa na mwelekeo wa kufanya maovu, nao wataketi kwenye meza moja wakiambiana uwongo. Lakini hakuna lolote litakalofanikiwa, kwa maana mwisho utakuja kwa wakati uliowekwa.+
28 “Na mfalme wa kaskazini atarudi katika nchi yake akiwa na mali nyingi, na moyo wake utapinga lile agano takatifu. Atatenda kwa mafanikio na kurudi katika nchi yake.
29 “Kwa wakati uliowekwa atarudi na kushambulia kusini. Lakini wakati huo mambo hayatakuwa kama yalivyokuwa mwanzoni, 30 kwa maana meli za Kitimu+ zitamshambulia, naye atanyenyekezwa.
“Atarudi na kumwaga shutuma* dhidi ya lile agano takatifu,+ naye atatenda kwa mafanikio; atarudi na kuwakazia fikira wale wanaoliacha agano takatifu. 31 Na majeshi yatasimama, kutoka kwake; nayo yatachafua patakatifu,+ ile ngome, na kuondoa ile dhabihu inayotolewa daima.*+
“Nao watasimamisha kile kitu chenye kuchukiza sana kinachosababisha ukiwa.+
32 “Na wale wanaotenda uovu dhidi ya lile agano, atawaongoza kwa maneno ya ujanja* waingie katika uasi imani. Lakini watu wanaomjua Mungu wao watakuwa imara na kutenda kwa mafanikio. 33 Na wale walio na ufahamu+ miongoni mwa watu watawasaidia wengi kupata uelewaji. Nao* watakwazwa kwa upanga na kwa mwali wa moto, kwa kutekwa na kwa kuporwa, kwa siku kadhaa. 34 Lakini watakapokwazwa, watapokea msaada kidogo; na wengi watajiunga nao kwa maneno ya ujanja.* 35 Na baadhi ya wale wenye ufahamu watakwazwa, ili kazi ya kuwasafisha watu ifanywe kwa sababu yao na kazi ya kuwatakasa na kuwafanya kuwa weupe+ mpaka wakati wa mwisho; kwa maana bado ni ya wakati uliowekwa.
36 “Mfalme huyo atafanya apendavyo, naye atajikweza na kujitukuza juu ya kila mungu; naye atasema mambo ya kushangaza dhidi ya Mungu wa miungu.+ Naye atafanikiwa mpaka shutuma itakapofikia mwisho; kwa sababu kilichoamuliwa lazima kitendeke. 37 Hatamjali Mungu wa baba zake; wala hatajali tamaa ya wanawake wala hatajali mungu mwingine yeyote, lakini atajitukuza mwenyewe juu ya kila mtu. 38 Badala ya Mungu wa baba zake atampa utukufu mungu wa ngome; na kwa kutumia dhahabu na fedha na mawe yenye thamani na vitu vinavyotamanika,* atampa utukufu mungu ambaye baba zake hawakumjua. 39 Naye atashinda ngome zilizoimarishwa kabisa akiwa pamoja na* mungu wa kigeni. Atawapa utukufu mwingi wale wanaomtambua,* naye atawafanya wawatawale watu wengi; na ataigawa ardhi kwa malipo.
40 “Wakati wa mwisho mfalme wa kusini atasukumana* naye, na mfalme wa kaskazini atamshambulia vikali kwa kutumia magari ya vita na wapanda farasi na meli nyingi; naye ataingia katika nchi hizo na kupita humo kama mafuriko. 41 Ataingia pia katika nchi ya lile Pambo,*+ na nchi nyingi zitakwazwa. Lakini hizi ndizo nchi zitakazoponyoka mikononi mwake: Edomu na Moabu na sehemu kuu ya Waamoni. 42 Naye ataendelea kuunyoosha mkono wake kwa nguvu dhidi ya nchi hizo; na nchi ya Misri haitaponyoka. 43 Naye atatawala hazina zilizofichwa za dhahabu na fedha na vitu vyote vinavyotamanika* vya Misri. Na Walibya na Waethiopia watafuata nyayo zake.*
44 “Lakini habari kutoka mashariki* na kutoka kaskazini zitamhangaisha, naye atatoka kwa hasira kali ili kuwaangamiza na kuwaua wengi. 45 Naye atapiga mahema yake ya kifalme* kati ya bahari kuu na mlima mtakatifu wa lile Pambo;*+ naye atasonga kufikia mwisho wake, na hakuna atakayemsaidia.
12 “Wakati huo Mikaeli*+ atasimama,* yule mkuu+ anayesimama kwa ajili ya watu wako.* Na kutakuwa na wakati wa taabu ambao haujawahi kamwe kutokea tangu kuanzishwa kwa taifa lolote mpaka wakati huo. Na wakati huo watu wako wataponyoka,+ kila mtu atakayepatikana ameandikwa katika kile kitabu.+ 2 Na wengi kati ya wale wanaolala usingizi katika mavumbi ya dunia wataamka, baadhi yao watapata uzima wa milele na wengine watapata shutuma na chuki ya milele.
3 “Na wale walio na ufahamu watang’aa sana kama anga la mbingu, na wale wanaowaleta wengi kwenye uadilifu watang’aa kama nyota, milele na milele.
4 “Lakini wewe, Danieli, yaweke siri maneno haya, na ukifunge kwa muhuri kitabu hiki mpaka wakati wa mwisho.+ Wengi watazunguka huku na huku,* na ujuzi wa kweli utakuwa mwingi.”+
5 Kisha mimi, Danieli, nikatazama na kuwaona wengine wawili wamesimama mahali hapo, mmoja kwenye ukingo huu wa kijito na yule mwingine kwenye ukingo wa pili wa kijito.+ 6 Kisha mmoja akamuuliza yule mwanamume aliyevaa mavazi ya kitani,+ aliyekuwa juu ya maji ya kijito: “Itachukua muda gani kufikia mwisho wa mambo haya ya kustaajabisha?” 7 Kisha nikamsikia yule mwanamume aliyevaa mavazi ya kitani, aliyekuwa juu ya maji ya kijito, alipokuwa akiinua mkono wake wa kulia na mkono wake wa kushoto kuelekea mbinguni na kuapa hivi kwa jina la Yule anayeishi milele:+ “Itakuwa ni kwa wakati uliowekwa, nyakati zilizowekwa, na nusu ya wakati.* Mara tu kuvunjwavunjwa kwa nguvu za watu watakatifu kutakapofikia mwisho,+ mambo haya yote yatafikia mwisho wake.”
8 Basi mimi, nilisikia, lakini sikuweza kuelewa;+ kwa hiyo nikauliza: “Ee bwana wangu, matokeo ya mambo haya yote yatakuwa nini?”
9 Akajibu: “Nenda, Danieli, kwa sababu maneno haya yanapaswa kuwekwa yakiwa siri na kutiwa muhuri mpaka wakati wa mwisho.+ 10 Wengi watajitakasa na kujifanya weupe nao watasafishwa.+ Na waovu watatenda uovu, na hakuna mwovu yeyote atakayeelewa; lakini wale walio na ufahamu wataelewa.+
11 “Na tangu wakati wa kuondolewa kwa ile dhabihu inayotolewa daima*+ na kusimamishwa kwa kile kitu kinachochukiza sana kinachosababisha ukiwa,+ kutakuwa na siku 1,290.
12 “Mwenye furaha ni yule anayeendelea kutarajia* na anayefika kwenye zile siku 1,335!
13 “Lakini wewe, endelea mpaka mwisho. Utapumzika, lakini utasimama kwa ajili ya fungu lako* mwishoni mwa zile siku.”+
Au “hekalu la.”
Yaani, Babilonia.
Au “hekalu la.”
Tnn., “wana wa Israeli.”
Tnn., “watoto.”
Au labda, “kulishwa.”
Tnn., “wana wa.”
Maana yake “Mwamuzi Wangu Ni Mungu.”
Maana yake “Yehova Ameonyesha Kibali.”
Huenda jina hili linamaanisha “Ni Nani Aliye Kama Mungu?”
Maana yake “Yehova Amesaidia.”
Yaani, majina ya Kibabiloni.
Tnn., “amwonyeshe Danieli kibali.”
Tnn., “watoto.”
Tnn., “Mtakifanya kichwa changu kiwe na.”
Tnn., “watoto.”
Tnn., “miili yao ilinenepa.”
Tnn., “watoto.”
Tnn., “watoto.”
Tnn., “roho yake ikahangaika.”
Yaani, kikundi kilichokuwa stadi katika ubashiri na unajimu.
Tnn., “roho yangu inahangaika.”
Sehemu ya Da 2:4b hadi 7:28 iliandikwa kwa Kiaramu.
Au labda, “maeneo ya takataka; marundo ya mavi.”
Au “katika nchi kavu.”
Tnn., “wenye mwili wa nyama.”
Au “milele hata milele.”
Au “udongo wa mfinyanzi (uliofinyangwa) uliochomwa.”
Au “uzao wa wanadamu,” yaani, watu wa kawaida.
Au “wilaya yote ya utawala ya.”
Au “wilaya ya utawala ya.”
Mita 27 hivi (futi 88). Angalia Nyongeza B14.
Mita 2.7 hivi (futi 8.8). Angalia Nyongeza B14.
Au “wilaya ya utawala ya.”
Au “wilaya za utawala.”
Au “wilaya za utawala.”
Au “kuwachongea.”
Au “wilaya ya utawala ya.”
Au “mtazamo wake ukabadilika kabisa.”
Au “haukuwazidi nguvu.”
Au “na kutoa miili yao.”
Au labda, “maeneo ya takataka; marundo ya mavi.”
Tnn., “akawafanikisha.”
Au “wilaya ya utawala ya.”
Yaani, wabashiri na wanajimu hodari.
Tnn., “wote wenye mwili.”
Au “kuuzuia mkono wake.”
Au “sura ya mfalme ikabadilika.”
Yaani, wabashiri na wanajimu hodari.
Au “mwanamume mwenye uwezo.”
Yaani, wabashiri na wanajimu hodari.
Tnn., “kufungua mafundo.”
Tnn., “kufungua mafundo.”
Tnn., “ufalme.”
Tnn., “mdomo.”
Au labda, “hakuna wanamuziki walioletwa.”
Tnn., “usingizi ulimkimbia.”
Au “waliomchongea.”
Au “enzi yake ni ya.”
Au “kujigamba.”
Au “kujigamba.”
Au “kwa kujigamba.”
Yaani, nyakati tatu na nusu.
Au “sura yangu ikabadilika.”
Au “jumba la mfalme la.”
Au “Susa.”
Au “wilaya ya utawala ya.”
Tnn., “mkono wake.”
Au “machweo ya jua.”
Tnn., “mkono wake.”
Au “mawio ya jua.”
Au “ule Urembo.”
Au “kile kitu kinachotolewa kila siku kikaondolewa.”
Au “kile kitu kinachotolewa kila siku.”
Au “kile kitu kinachotolewa kila siku.”
Au “aliye stadi wa hila.”
Au “Ataleta uharibifu wa kutisha.”
Au labda, “bila onyo.”
Au “wakati ujao ulio mbali.”
Yaani, vitabu vitakatifu.
Au “hukumu.”
Tnn., “waamuzi wetu waliotuhukumu.”
Au “hatujautuliza uso wa.”
Au “uaminifu.”
Au “anayependwa sana; anayeheshimiwa sana.”
Yaani, majuma 70 ya miaka.
Tnn., “nabii.”
Au “Patakatifu Zaidi.”
Au “Mtiwa-Mafuta.”
Tnn., “atakatiliwa mbali.”
Tnn., “Hidekeli.”
Au “anayependwa sana; anayeheshimiwa sana.”
Maana yake “Ni Nani Aliye Kama Mungu?”
Au “mkuu wa cheo cha kwanza.”
Au “anayependwa sana; anayeheshimiwa sana.”
Au “kuwa kama ngome kwake.”
Au “watainuka.”
Au “kizazi chake kijacho.”
Au “sanamu zao za kuyeyushwa.”
Au “vyenye thamani.”
Inaonekana ni mfalme wa kusini.
Au “wana wa wanyang’anyi.”
Tnn., “mikono ya kusini haitasimama.”
Au “ule Urembo.”
Tnn., “atakaza uso wake kabisa.”
Inaonekana ni mfalme wa kaskazini.
Huenda ni “mtoza ushuru.” Au “msimamizi wa kazi.”
Au “anayechukiza.”
Au labda, “bila onyo.”
Au “hila.”
Tnn., “mikono ya mafuriko itafagiliwa.”
Au labda, “Bila onyo.”
Au “wilaya ya utawala.”
Tnn., “unono.”
Au “kuelekeza ghadhabu yake.”
Au “kile kitu kinachotolewa kila siku.”
Au “kurairai; yasiyo ya unyoofu.”
Yaani, walio na ufahamu.
Au “kurairai; yasiyo ya unyoofu.”
Au “vyenye thamani.”
Au “akisaidiwa na.”
Au labda, “Atampa utukufu mwingi yeyote anayemtambua.”
Au “atamenyana.”
Au “ule Urembo.”
Au “vyenye thamani.”
Au “watamfuata.”
Au “mawio ya jua.”
Au “ya kifahari.”
Au “ule Urembo.”
Maana yake “Ni Nani Aliye Kama Mungu?”
Au “atainuka.”
Tnn., “wana wa watu wako.”
Au “watakichunguza [yaani, kitabu hiki] kwa makini.”
Yaani, nyakati tatu na nusu.
Au “kile kitu kinachotolewa kila siku.”
Au “anayengojea kwa hamu kubwa.”
Au “mahali pako ulipogawiwa.”