Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt Matendo 1:1-28:31
  • Matendo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Matendo
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Matendo

MATENDO YA MITUME

1 Lile simulizi la kwanza, ewe Theofilo, niliandika kuhusu mambo yote ambayo Yesu alianza kufanya na kufundisha+ 2 mpaka siku aliyochukuliwa kwenda juu,+ baada ya kuwapa mitume aliowachagua maagizo kupitia roho takatifu.+ 3 Baada ya kuteseka, alijionyesha kwao akiwa hai kupitia uthibitisho mwingi wenye kusadikisha.+ Walimwona kwa siku 40, naye alizungumza nao kuhusu Ufalme wa Mungu.+ 4 Alipokuwa akikutana nao aliwaagiza hivi: “Msiondoke Yerusalemu,+ bali endeleeni kusubiri kile ambacho Baba ameahidi,+ ambacho mlinisikia nikisema kukihusu; 5 kwa maana Yohana, kwa kweli, alibatiza kwa maji, lakini ninyi mtabatizwa kwa roho takatifu+ baada ya siku chache.”

6 Basi, walipokusanyika, wakamuuliza: “Bwana, je, unaurudisha ufalme kwa Israeli wakati huu?”+ 7 Akawaambia: “Si juu yenu kujua nyakati au majira ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe.+ 8 Lakini roho takatifu itakapokuja juu yenu mtapokea nguvu,+ nanyi mtakuwa mashahidi+ wangu katika Yerusalemu,+ katika Yudea yote na Samaria,+ na mpaka sehemu ya mbali zaidi* ya dunia.”+ 9 Baada ya kusema mambo hayo, wakiwa wanatazama, akainuliwa juu na wingu likamfunika nao hawakumwona tena.+ 10 Nao walipokuwa wakitazama angani akiwa anaenda, ghafla wanaume wawili wenye mavazi meupe+ wakasimama kando yao 11 na kusema: “Wanaume wa Galilaya, kwa nini mnasimama mkitazama angani? Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda angani atakuja vivyo hivyo kama vile ambavyo mmemwona akienda angani.”

12 Kisha wakarudi Yerusalemu+ kutoka kwenye Mlima wa Mizeituni, ulio karibu na Yerusalemu, umbali wa safari ya siku ya sabato. 13 Walipofika, walienda kwenye chumba cha juu, walipokuwa wakikaa. Walikuwa Petro, Yohana, Yakobo, Andrea, Filipo, Tomasi, Bartholomayo, Mathayo, Yakobo mwana wa Alfayo, Simoni mwenye bidii, na Yuda mwana wa Yakobo.+ 14 Wote hawa walidumu katika sala kwa kusudi moja, wakiwa pamoja na wanawake+ fulani na Maria mama ya Yesu, pamoja na ndugu za Yesu.+

15 Katika siku hizo Petro akasimama kati ya akina ndugu (kwa ujumla idadi ya* watu ilikuwa karibu 120) na kusema: 16 “Wanaume, akina ndugu, ilikuwa lazima andiko litimizwe, ambalo roho takatifu ilisema kinabii kupitia Daudi kumhusu Yuda,+ aliyewaongoza wale waliomkamata Yesu.+ 17 Kwa maana alihesabiwa miongoni mwetu+ naye alipata fungu katika huduma hii. 18 (Mtu huyo alinunua shamba kwa mshahara wa ukosefu wa uadilifu,+ akaanguka kichwa kwanza, mwili wake ukapasuka* na matumbo yake yote yakamwagika.+ 19 Wakaaji wote wa Yerusalemu wakajua jambo hilo, hivi kwamba shamba hilo likaitwa kwa lugha yao Akeldama, yaani, “Shamba la Damu.”) 20 Kwa maana imeandikwa katika kitabu cha Zaburi, ‘Makao yake yabaki ukiwa, na pasiwe na mkaaji yeyote humo,’+ na, ‘Mtu mwingine na achukue cheo chake cha uangalizi.’+ 21 Kwa hiyo inafaa kwamba mmoja wa wanaume walioandamana nasi wakati wote ambao Bwana Yesu alifanya kazi zake* miongoni mwetu, 22 kuanzia alipobatizwa na Yohana+ mpaka siku alipochukuliwa kutoka kwetu kwenda juu,+ mmoja wa wanaume hao anapaswa kuwa shahidi pamoja nasi kuhusu ufufuo wake.”+

23 Kwa hiyo wakapendekeza watu wawili, Yosefu aliyeitwa pia Barsaba au Yusto, na Mathia. 24 Ndipo wakasali wakisema: “Wewe, Ee Yehova,* unayejua mioyo ya wote,+ onyesha ni nani kati ya watu hawa wawili ambaye umemchagua 25 achukue mahali pa huduma na utume huu, ambao Yuda aliuacha na kwenda mahali pake mwenyewe.”+ 26 Basi wakawapigia kura,+ na kura ikamwangukia Mathia, naye akahesabiwa* pamoja na wale mitume 11.

2 Basi siku ya Sherehe ya Pentekoste+ ilipokuwa ikiendelea, wote walikuwa pamoja mahali palepale. 2 Ghafla kukatokea kelele kutoka mbinguni, kama ya upepo wenye nguvu unaovuma, nao ukaijaza nyumba yote ambamo walikuwa wameketi.+ 3 Nao wakaona ndimi kama za moto, nazo zikagawanyika, na mmoja ukatua juu ya kila mmoja wao, 4 wote wakajazwa roho takatifu,+ wakaanza kusema katika lugha* mbalimbali, kama roho ilivyowawezesha kusema.+

5 Wakati huo Wayahudi waliomwogopa Mungu kutoka kila taifa lililo chini ya mbingu walikuwa wakikaa Yerusalemu.+ 6 Basi sauti hiyo ilipotokea, umati ukakusanyika na kustaajabu, kwa sababu kila mmoja wao aliwasikia wakiongea katika lugha yake mwenyewe. 7 Kwa kweli, walishangaa sana na kusema: “Tazama, hawa wote wanaoongea ni Wagalilaya,+ sivyo? 8 Inakuwaje kwamba kila mmoja wetu anasikia lugha yake ya asili?* 9 Waparthi, Wamedi,+ na Waelami,+ wakaaji wa Mesopotamia, Yudea na Kapadokia, Ponto na mkoa wa Asia,+ 10 Frigia, Pamfilia, Misri, na maeneo ya Libya karibu na Kirene, wakaaji wa muda wa kutoka Roma, Wayahudi na pia wageuzwa imani,+ 11 Wakrete, na Waarabu—tunawasikia wakisema katika lugha zetu kuhusu mambo makuu ya Mungu.” 12 Ndiyo, wote wakashangaa na kustaajabu, wakaulizana: “Jambo hili linamaanisha nini?” 13 Hata hivyo, wengine wakawadhihaki na kusema: “Wamejaa divai tamu.”*

14 Lakini Petro akasimama pamoja na wale 11+ na kuzungumza nao kwa sauti kubwa akisema: “Watu wa Yudea nanyi nyote wakaaji wa Yerusalemu, jueni jambo hili nanyi msikilize kwa makini maneno yangu. 15 Kwa kweli, watu hawa hawajalewa kama mnavyodhani, kwa maana ni saa tatu mchana.* 16 Badala yake, hili ndilo lililosemwa kupitia nabii Yoeli: 17 ‘“Na katika siku za mwisho,” Mungu asema, “Nitaimimina sehemu ya roho yangu juu ya kila aina ya mwili, na wana wenu na mabinti wenu watatoa unabii, nao wanaume wenu vijana wataona maono, na wanaume wenu wazee wataota ndoto,+ 18 na hata juu ya watumwa wangu wa kiume na watumwa wa kike nitaimimina sehemu ya roho yangu siku hizo, nao watatoa unabii.+ 19 Nami nitafanya mambo ya ajabu* juu mbinguni na ishara chini duniani—damu na moto na mawingu ya moshi. 20 Jua litatiwa giza na mwezi utatiwa damu kabla ya kuja kwa ile siku ya Yehova* iliyo kuu na yenye utukufu. 21 Na kila mtu anayeliitia jina la Yehova* ataokolewa.”’+

22 “Watu wa Israeli, sikieni maneno haya: Yesu Mnazareti alikuwa mwanamume ambaye Mungu alimwonyesha hadharani kwenu kupitia matendo yenye nguvu na mambo ya ajabu* na ishara ambazo Mungu alifanya kupitia kwake miongoni mwenu,+ kama mnavyojua. 23 Mwanamume huyu, aliyekabidhiwa kupitia mapenzi yaliyoamuliwa* na ujuzi wa awali wa Mungu,+ mlimfunga kwenye mti kupitia mkono wa waasi sheria, nanyi mkamuua.+ 24 Lakini Mungu alimfufua+ kwa kumfungua kutoka katika maumivu makali ya* kifo, kwa sababu haingewezekana kifo kiendelee kumshika.+ 25 Kwa kuwa Daudi anasema hivi kumhusu: ‘Nimemweka Yehova* mbele yangu* daima, kwa maana yuko mkono wangu wa kulia ili nisitikiswe kamwe. 26 Kwa hiyo moyo wangu ulichangamka na ulimi wangu ukashangilia sana. Nami nitaishi* katika tumaini; 27 kwa sababu hutaniacha* Kaburini,* wala hutamruhusu mshikamanifu wako aone uharibifu.*+ 28 Umenijulisha njia za uzima; utanijaza shangwe nyingi mbele zako.’*+

29 “Wanaume, akina ndugu, inaruhusika nizungumze nanyi kwa uhuru wa kusema kumhusu Daudi kichwa cha familia, kwamba alikufa, akazikwa,+ na kaburi lake liko hapa kwetu mpaka leo. 30 Kwa sababu alikuwa nabii na alijua kwamba Mungu alikuwa amemwapia kwa kiapo kwamba angemfanya mmoja wa wazao wake* aketi kwenye kiti chake cha ufalme,+ 31 aliona mapema na kusema kuhusu ufufuo wa Kristo, kwamba hakuachwa katika Kaburi* wala mwili wake haukuona uharibifu.*+ 32 Mungu alimfufua, Yesu huyu, na sisi sote ni mashahidi wa jambo hilo.+ 33 Kwa hiyo, kwa sababu aliinuliwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu+ na kupokea roho takatifu iliyoahidiwa kutoka kwa Baba,+ amemimina hiki mnachoona na kusikia. 34 Kwa kuwa Daudi hakupanda mbinguni, bali yeye mwenyewe anasema, ‘Yehova* alimwambia Bwana wangu: “Keti kwenye mkono wangu wa kuume 35 mpaka niwaweke maadui wako kuwa kiti cha miguu yako.”’+ 36 Kwa hiyo, nyumba yote ya Israeli na ijue kwa hakika kwamba Mungu alimfanya Bwana+ na pia Kristo, Yesu huyu ambaye ninyi mlimuua kwenye mti.”+

37 Basi waliposikia hilo, walichomwa moyoni, nao wakamwambia Petro na wale mitume wengine: “Wanaume, akina ndugu, tufanye nini?” 38 Petro akawaambia: “Tubuni,+ na kila mmoja wenu abatizwe+ katika jina la Yesu Kristo ili msamehewe dhambi zenu,+ nanyi mtapokea zawadi ya bure ya roho takatifu. 39 Kwa maana ahadi+ hii ni kwa ajili yenu na watoto wenu, na kwa wale wote walio mbali, kwa wote ambao huenda Yehova* Mungu wetu akawaita kwake.”+ 40 Akaendelea kuwahimiza na kutoa ushahidi kamili kwa maneno mengine mengi, akisema: “Okoleweni kutoka katika kizazi hiki kilichopotoka.”+ 41 Basi wale waliokubali neno lake kwa furaha wakabatizwa,+ na siku hiyo karibu watu 3,000 wakaongezwa.*+ 42 Nao wakaendelea kujitoa kwa bidii kwa fundisho la mitume, kushirikiana pamoja,* kula milo,+ na kusali.+

43 Kwa kweli, kila mtu akawa* na hofu, nao mitume wakaanza kufanya mambo mengi ya ajabu* na ishara nyingi.+ 44 Wale wote ambao sasa walikuwa waamini walikusanyika pamoja na wakashirikiana katika mambo yote, 45 nao walikuwa wakiuza mali zao+ na vitu walivyomiliki na kuwagawia wote pesa walizopata, kulingana na uhitaji wa kila mtu.+ 46 Kila siku walihudhuria daima kwenye hekalu kwa kusudi moja, nao walikula milo yao katika nyumba mbalimbali na kushiriki chakula chao kwa shangwe nyingi na kwa moyo mweupe, 47 wakimsifu Mungu na kupata kibali kwa watu wote. Wakati uleule Yehova* akaendelea kuwaongezea kila siku watu waliokuwa wakiokolewa.+

3 Basi Petro na Yohana walikuwa wakipanda kwenda hekaluni wakati wa saa ya sala, yaani, saa tisa,* 2 na mwanamume fulani aliyekuwa kilema tangu kuzaliwa alikuwa amebebwa. Kila siku walimweka karibu na lango la hekalu lililoitwa Lango Zuri, ili aombe zawadi za rehema kutoka kwa wale waliokuwa wakiingia hekaluni. 3 Alipowaona Petro na Yohana wakiwa karibu kuingia hekaluni, akaanza kuomba zawadi za rehema. 4 Lakini Petro, pamoja na Yohana, wakamtazama moja kwa moja na kumwambia: “Tuangalie.” 5 Kwa hiyo akawaangalia, akitarajia kupata kitu kutoka kwao. 6 Hata hivyo, Petro akasema: “Sina fedha wala dhahabu, lakini kile nilicho nacho ndicho ninachokupa. Katika jina la Yesu Kristo Mnazareti, tembea!”+ 7 Ndipo akamshika mkono wa kulia na kumwinua.+ Papo hapo miguu yake na vifundo vya miguu yake vikafanywa imara;+ 8 akasimama mara moja,+ akaanza kutembea na kuingia nao hekaluni, akitembea na kurukaruka akimsifu Mungu. 9 Watu wote wakamwona akitembea huku akimsifu Mungu. 10 Wakaanza kutambua kwamba huyu ndiye mtu aliyekuwa akiketi kwenye Lango Zuri la hekalu+ akisubiri zawadi za rehema, nao wakashangaa sana na kushangilia kuhusu jambo lililotokea.

11 Mtu huyo akiwa bado amewashika Petro na Yohana, watu wote wakawakimbilia pamoja kwenye sehemu iliyoitwa Safu ya Nguzo za Sulemani,+ wakiwa wameshangaa sana. 12 Petro alipoona jambo hilo, akawaambia watu hao: “Watu wa Israeli, kwa nini mnastaajabishwa na jambo hili, na kwa nini mnatutazama kana kwamba tumemfanya atembee kwa nguvu zetu au kwa sababu ya ujitoaji-kimungu?* 13 Mungu wa Abrahamu na wa Isaka na wa Yakobo,+ Mungu wa mababu zetu, amemtukuza Mtumishi wake,+ Yesu,+ ambaye ninyi mlimkabidhi+ na kumkana mbele ya Pilato, ingawa alikuwa ameamua kumfungua. 14 Ndiyo, mlimkana huyo aliye mtakatifu na mwadilifu, nanyi mkaomba mpewe mwanamume aliyekuwa muuaji,+ 15 lakini mkamuua Wakili Mkuu wa uzima.+ Hata hivyo, Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, nasi ni mashahidi wa jambo hilo.+ 16 Kupitia jina lake, na kwa imani yetu katika jina lake, mtu huyu mnayemwona na kumfahamu amefanywa awe mwenye nguvu. Imani kupitia kwake imemfanya mtu huyu awe mwenye afya kamili, mbele yenu nyote. 17 Na sasa, akina ndugu, ninajua kwamba mlitenda kwa kutojua,+ kama vile watawala wenu pia walivyotenda.+ 18 Lakini kwa njia hiyo Mungu ametimiza mambo aliyotangaza mapema kupitia kinywa cha manabii wote, kwamba Kristo wake angeteseka.+

19 “Kwa hiyo, tubuni+ na mgeuke+ ili dhambi zenu zifutwe,+ ili majira yenye kuburudisha yaje kutoka kwa Yehova mwenyewe,* 20 naye amtume Kristo aliyewekwa rasmi kwa ajili yenu, yaani, Yesu. 21 Naye lazima abaki mbinguni mpaka nyakati za kurudishwa kwa mambo yote ambayo Mungu alisema kupitia kinywa cha manabii wake watakatifu walioishi zamani. 22 Kwa kweli, Musa alisema: ‘Yehova* Mungu wenu atawainulia nabii kama mimi kutoka kati ya ndugu zenu.+ Ni lazima msikilize kile atakachowaambia.+ 23 Kwa kweli, yeyote* ambaye hatamsikiliza Nabii huyo ataangamizwa kutoka kati ya watu.’+ 24 Manabii wote kuanzia Samweli na wale waliofuata, wengi ambao wamesema, wametangaza waziwazi pia kuhusu siku hizi.+ 25 Ninyi ndio wana wa manabii na wa agano ambalo Mungu alifanya na mababu zenu,+ alipomwambia Abrahamu: ‘Kupitia uzao wako,* familia zote za dunia zitabarikiwa.’+ 26 Baada ya Mungu kumwinua Mtumishi wake, alimtuma kwenu kwanza+ ili awabariki ninyi kwa kumgeuza kila mmoja wenu aache matendo yake maovu.”

4 Hao wawili walipokuwa wakizungumza na watu, makuhani, kapteni wa hekalu, na Masadukayo+ wakawajia. 2 Walikuwa wameudhika kwa sababu mitume walikuwa wakiwafundisha watu na kutangaza waziwazi kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa kutoka kwa wafu.*+ 3 Basi wakawakamata na kuwaweka kizuizini+ mpaka siku iliyofuata, kwa maana tayari ilikuwa jioni. 4 Hata hivyo, wengi waliokuwa wamesikiliza maneno hayo wakaamini, na idadi ya wanaume ikawa karibu 5,000.+

5 Siku iliyofuata watawala wao, wazee, na waandishi wakakusanyika pamoja huko Yerusalemu 6 pamoja na Anasi+ mkuu wa makuhani, Kayafa,+ Yohana, Aleksanda, na wote waliokuwa watu wa ukoo wa mkuu wa makuhani. 7 Wakawasimamisha Petro na Yohana katikati yao na kuanza kuwauliza: “Mlifanya jambo hilo kwa nguvu gani au katika jina la nani?” 8 Ndipo Petro, akiwa amejaa roho takatifu,+ akawaambia:

“Watawala wa watu na wazee, 9 ikiwa tunahojiwa leo kuhusu tendo jema alilofanyiwa mtu huyu aliyekuwa kilema,+ na ikiwa mnataka kujua aliyemponya, 10 na ijulikane kwenu nyote na kwa watu wote wa Israeli kwamba katika jina la Yesu Kristo Mnazareti,+ ambaye mlimuua kwenye mti+ lakini Mungu akamfufua kutoka kwa wafu,+ kupitia kwake mtu huyu anasimama hapa mbele yenu akiwa ameponywa. 11 Hilo ndilo ‘jiwe ambalo ninyi wajenzi mlilitendea kana kwamba halina maana nalo limekuwa jiwe kuu la pembeni.’*+ 12 Zaidi ya hayo, hakuna wokovu katika mwingine yeyote, kwa maana hakuna jina lingine+ chini ya mbingu walilopewa wanadamu ambalo kupitia hilo tunaweza kuokolewa.”+

13 Walipoona Petro na Yohana wakizungumza kwa ujasiri, ingawa walikuwa watu wasio na elimu* na wa kawaida tu,+ wakashangaa. Nao wakatambua kwamba walikuwa pamoja na Yesu.+ 14 Walipokuwa wakimtazama yule mtu aliyekuwa ameponywa, akiwa amesimama pamoja nao,+ hawakuwa na jambo la kusema.+ 15 Basi wakawaamuru waende nje ya jumba la Sanhedrini, kisha wakaanza kushauriana, 16 wakisema: “Tufanye nini na watu hawa?+ Kwa sababu kwa kweli ishara kubwa imetukia kupitia kwao ambayo imejulikana na wakaaji wote wa Yerusalemu,+ nasi hatuwezi kuikana. 17 Ili jambo hili lisizidi kusambazwa kati ya watu, basi tuwatishe na kuwaambia wasizungumze tena na mtu yeyote kwa msingi wa jina hilo.”+

18 Ndipo wakawaita na kuwaamuru wasiseme lolote wala kufundisha kwa msingi wa jina la Yesu. 19 Lakini Petro na Yohana wakawajibu: “Kama ni sawa machoni pa Mungu kuwasikiliza ninyi badala ya Mungu, hukumuni ninyi wenyewe. 20 Lakini sisi hatuwezi kuacha kusema kuhusu mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.”+ 21 Basi baada ya kuwatisha zaidi, wakawafungua, kwa vile hawakupata msingi wowote wa kuwaadhibu na kwa kuwa waliwaogopa watu,+ kwani wote walikuwa wakimtukuza Mungu kwa sababu ya jambo lililokuwa limetukia. 22 Kwa maana yule mtu ambaye alifanyiwa muujiza huo* wa kuponywa alikuwa na umri wa zaidi ya miaka 40.

23 Baada ya kufunguliwa, wakaenda kwa watu wao na kuwaeleza mambo waliyoambiwa na wakuu wa makuhani na wazee. 24 Waliposikia hayo, wote kwa pamoja wakasali kwa Mungu wakisema kwa sauti kubwa:

“Bwana Mwenye Enzi Kuu, wewe Ndiye uliyeumba mbingu, dunia, bahari, na vitu vyote vilivyomo,+ 25 nawe ulisema kupitia roho takatifu kwa kinywa cha babu yetu Daudi,+ mtumishi wako: ‘Kwa nini mataifa yalikuwa na msukosuko na watu wakatafakari mambo matupu? 26 Wafalme wa dunia walijipanga nao watawala wakakusanyika pamoja kama kitu kimoja dhidi ya Yehova* na dhidi ya mtiwa-mafuta wake.’*+ 27 Kwa kweli Herode na Pontio Pilato+ pamoja na watu wa mataifa na watu wa Israeli walikusanyika katika jiji hili dhidi ya mtumishi wako mtakatifu Yesu, ambaye ulimtia mafuta,+ 28 ili wafanye yale ambayo mkono na shauri lako liliazimia awali yatukie.+ 29 Na sasa, Yehova,* angalia vitisho vyao, nawe uwawezeshe watumwa wako waendelee kutangaza neno lako kwa ujasiri wote, 30 huku ukinyoosha mkono wako ili uponye, na huku ishara na mambo ya ajabu* yakitukia+ kupitia jina la mtumishi wako mtakatifu Yesu.”+

31 Na baada ya kutoa dua,* mahali walipokuwa wamekusanyika pakatikiswa, na kila mmoja wao akajazwa roho takatifu+ nao walikuwa wakitangaza neno la Mungu kwa ujasiri.+

32 Isitoshe, umati uliokuwa umeamini ulikuwa na moyo na nafsi* moja, na hakuna hata mmoja wao aliyeona vitu vyake kuwa mali yake mwenyewe, bali walishiriki pamoja vitu vyote walivyokuwa navyo.+ 33 Na kwa nguvu nyingi, mitume wakaendelea kutoa ushahidi kuhusu ufufuo wa Bwana Yesu,+ na fadhili zisizostahiliwa zilikuwa pamoja nao kwa kadiri kubwa. 34 Kwa kweli, hakuna yeyote kati yao aliyekuwa na uhitaji,+ kwa maana wote waliokuwa na mashamba au nyumba walikuwa wakiuza na kuleta thamani ya kile walichouza, 35 na kukiweka miguuni pa mitume.+ Kisha kila mmoja aligawiwa kulingana na uhitaji wake.+ 36 Kwa hiyo Yosefu, ambaye pia mitume walimwita Barnaba+ (jina ambalo linapotafsiriwa linamaanisha, “Mwana wa Faraja”), Mlawi, mzaliwa wa Kipro, 37 alikuwa na shamba, akaliuza, akaleta pesa na kuziweka miguuni pa mitume.+

5 Hata hivyo, mwanamume fulani aliyeitwa Anania, pamoja na Safira mke wake, waliuza mali. 2 Lakini akajiwekea kisiri kiasi fulani, mke wake pia akijua jambo hilo, naye akaleta sehemu fulani tu na kuiweka miguuni pa mitume.+ 3 Lakini Petro akamuuliza: “Anania, kwa nini Shetani amekupa ujasiri wa kuidanganya+ roho takatifu+ ukajiwekea kisiri kiasi fulani cha bei ya shamba? 4 Kabla ya kuliuza, je, halikuwa mali yako? Na baada ya kuliuza, je, pesa hizo hazikuwa mikononi mwako? Kwa nini umewaza tendo kama hili moyoni mwako? Umedanganya si wanadamu, bali Mungu.” 5 Anania aliposikia maneno hayo, akaanguka chini akafa. Na wote waliosikia jambo hilo wakaogopa sana. 6 Basi vijana wakasimama, wakamfunga kwa vitambaa, wakamtoa nje, na kumzika.

7 Sasa baada ya muda wa saa tatu hivi, mke wake akaingia bila kujua kilichokuwa kimetokea. 8 Petro akamuuliza: “Niambie, je, ninyi wawili mliuza shamba kwa kiasi hiki?” Akajibu: “Ndiyo, kwa kiasi hicho.” 9 Kwa hiyo Petro akamwambia: “Kwa nini ninyi wawili mlikubaliana kuijaribu roho ya Yehova?* Tazama! Miguu ya wale waliomzika mume wako, ipo mlangoni, nao watakubeba na kukutoa nje.” 10 Papo hapo akaanguka chini miguuni pa Petro akafa. Wale vijana walipoingia walikuta amekufa, wakamtoa nje na kumzika kando ya mume wake. 11 Basi kutaniko lote na wote waliosikia kuhusu mambo hayo wakaogopa sana.

12 Isitoshe, kupitia mikono ya mitume ishara nyingi na mambo ya ajabu* yakaendelea kutukia kati ya watu;+ na wote walikuwa wakikutana kwenye Safu ya Nguzo za Sulemani.+ 13 Kwa kweli, hakuna yeyote kati ya wale wengine aliyekuwa na ujasiri wa kujiunga nao; hata hivyo, watu walikuwa wakiwasifu. 14 Isitoshe, wale waliomwamini Bwana wakazidi kuongezeka, idadi kubwa ya wanaume na wanawake.+ 15 Hata wakawaleta wagonjwa kwenye njia kuu na kuwalaza kwenye vitanda vidogo na mikeka, ili Petro akipita hapo, angalau kivuli chake kiwaangukie baadhi yao.+ 16 Pia, umati kutoka kwenye majiji yaliyokuwa karibu na Yerusalemu ukazidi kuja, ukiwa umewabeba wagonjwa na wale waliosumbuliwa na roho waovu, nao wote wakaponywa.

17 Lakini kuhani mkuu akasimama, na wote waliokuwa pamoja naye, ambao walikuwa wafuasi wa madhehebu ya Masadukayo, nao walikuwa wamejaa wivu. 18 Basi wakawakamata mitume na kuwafunga katika jela ya watu wote.+ 19 Lakini usiku, malaika wa Yehova* akaifungua milango ya gereza,+ akawatoa nje na kuwaambia: 20 “Nendeni mkasimame hekaluni, na mwendelee kuwaambia watu maneno yote kuhusu maisha haya.” 21 Baada ya kusikia hilo, wakaingia hekaluni wakati wa mapambazuko na kuanza kufundisha.

Basi kuhani mkuu na wale waliokuwa pamoja naye walipofika, wakakusanya Sanhedrini na kusanyiko lote la wazee wa wana wa Israeli, nao wakawatuma watu kwenye jela ili wawalete mitume mbele yao. 22 Lakini wale maofisa walipofika huko, hawakuwakuta gerezani. Basi wakarudi na kutoa taarifa, 23 wakisema: “Tuliikuta jela ikiwa imefungwa kabisa na walinzi wakiwa wamesimama kwenye milango, lakini tulipoifungua hatukumkuta mtu yeyote ndani.” 24 Basi, kapteni wa hekalu na wakuu wa makuhani waliposikia maneno hayo, walifadhaika sana kwa kuwa hawakujua jambo hilo lingekuwa na matokeo gani. 25 Lakini mtu fulani akaja na kuwaambia: “Tazameni! Wale watu mliowafunga gerezani wako hekaluni, wakiwa wamesimama wakiwafundisha watu.” 26 Ndipo kapteni akaenda pamoja na maofisa wake na kuwaleta bila kutumia nguvu, kwa maana waliogopa watu watawapiga mawe.+

27 Basi wakawaleta na kuwasimamisha mbele ya Sanhedrini. Kisha kuhani mkuu akawahoji 28 akisema: “Tuliwakataza kabisa msifundishe kwa msingi wa jina hili,+ na bado tazama! mmejaza Yerusalemu fundisho lenu, nanyi mmeazimia kuileta damu ya mtu huyu juu yetu.”+ 29 Petro na wale mitume wengine wakajibu: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.+ 30 Mungu wa mababu zetu alimfufua Yesu, ambaye ninyi mlimuua, kwa kumtundika kwenye mti.+ 31 Mungu alimwinua huyo kuwa Wakili Mkuu+ na Mwokozi+ kwenye mkono wake wa kuume,+ ili kuwapa Israeli toba na msamaha wa dhambi zao.+ 32 Nasi ni mashahidi wa mambo hayo,+ na pia roho takatifu,+ ambayo Mungu amewapa wale wanaomtii akiwa mtawala.”

33 Waliposikia hayo, wakakasirika sana* nao wakataka kuwaangamiza. 34 Lakini Farisayo mmoja aitwaye Gamalieli+ akasimama katika Sanhedrini; alikuwa mwalimu wa Sheria aliyeheshimiwa na watu wote, naye akaamuru watu hao watolewe nje kwa muda mfupi. 35 Kisha akawaambia: “Wanaume wa Israeli, iweni waangalifu kuhusu jambo mnalokusudia kuwatendea watu hawa. 36 Kwa mfano, kabla ya siku hizi Theuda alisimama akidai kwamba yeye ni mtu wa maana, na wanaume kadhaa, karibu 400, wakajiunga na chama chake. Lakini aliangamizwa, na wafuasi wake wote wakatawanyika na kwisha. 37 Baada yake, Yuda Mgalilaya akainuka katika zile siku za uandikishaji, naye akawa na wafuasi. Mtu huyo pia aliangamia, na wafuasi wake wote wakatawanyika. 38 Basi chini ya hali zilizopo, ninawaambia, msiingilie mambo ya watu hawa, bali waacheni. Kwa maana, ikiwa mpango huu au kazi hii ni ya wanadamu, itaangamizwa; 39 lakini ikiwa imetoka kwa Mungu, hamtaweza kuwaangamiza.+ La sivyo, huenda ikawa mnapigana na Mungu mwenyewe.”+ 40 Ndipo wakasikiliza ushauri wake, wakawaita mitume, wakawapiga viboko,+ na kuwaagiza waache kusema kwa msingi wa jina la Yesu, kisha wakawaacha waende.

41 Basi wakatoka mbele ya Sanhedrini, wakishangilia+ kwa sababu walikuwa wamestahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake. 42 Na kila siku hekaluni na nyumba kwa nyumba+ wakaendelea kufundisha na kutangaza habari njema kumhusu Kristo Yesu bila kuacha.+

6 Basi katika siku hizo, wanafunzi walipokuwa wakiongezeka, Wayahudi waliozungumza Kigiriki walianza kulalamika kuhusu Wayahudi waliozungumza Kiebrania, kwa sababu wajane wao walikuwa wakipuuzwa katika ugawaji wa kila siku.+ 2 Basi wale 12 wakauita umati wa wanafunzi na kuwaambia: “Si vema* sisi tuache neno la Mungu ili kugawa chakula mezani.+ 3 Basi akina ndugu, jichagulieni kati yenu wanaume saba wenye sifa nzuri,+ waliojaa roho na hekima,+ ili tuwaweke rasmi wafanye kazi hii muhimu;+ 4 lakini sisi tutajitoa kwa sala na huduma ya neno.” 5 Wanafunzi wote wakakubaliana na jambo walilosema, nao wakamchagua Stefano, mwanamume aliyejaa imani na roho takatifu, vilevile Filipo,+ Prokoro, Nikanori, Timoni, Parmena, na Nikolao, mgeuzwa-imani wa Antiokia. 6 Wakawaleta kwa mitume, na baada ya kusali, wakaweka mikono juu yao.+

7 Kwa hiyo, neno la Mungu likazidi kuenea,+ na idadi ya wanafunzi ikazidi kuongezeka sana+ huko Yerusalemu; na umati mkubwa wa makuhani wakawa waamini.+

8 Sasa Stefano, akiwa amejaa kibali cha Mungu na nguvu, alikuwa akifanya mambo makubwa ya ajabu* na ishara kati ya watu. 9 Lakini watu fulani wa Sinagogi la Watu Waliowekwa Huru wakaja mbele, pamoja na Wakirene na Waaleksandria, na wengine kutoka Kilikia na Asia, ili kubishana na Stefano. 10 Lakini hawakuweza kumshinda kwa sababu ya hekima yake na roho iliyomwongoza kusema.+ 11 Ndipo wakawashawishi watu kwa siri waseme: “Tumemsikia akisema maneno ya kumkufuru Musa na Mungu.” 12 Nao wakawachochea watu, wazee, na waandishi, wakamjia ghafla, wakamkamata kwa nguvu na kumpeleka kwenye Sanhedrini. 13 Wakawaleta mbele mashahidi wa uwongo, waliosema: “Mtu huyu haachi kusema mambo yasiyofaa kuhusu mahali hapa patakatifu na kuhusu Sheria. 14 Kwa mfano, tumemsikia akisema kwamba huyu Yesu Mnazareti atapaangusha mahali hapa na kuzibadili desturi ambazo Musa alitukabidhi.”

15 Wote waliokuwa wameketi katika Sanhedrini wakamkazia macho, nao wakaona uso wake ukiwa kama uso wa malaika.

7 Lakini kuhani mkuu akasema: “Je, mambo hayo ni ya kweli?” 2 Stefano akajibu: “Wanaume, akina ndugu na akina baba, sikilizeni. Mungu wa utukufu alimtokea babu yetu Abrahamu alipokuwa Mesopotamia, kabla hajaanza kuishi Harani,+ 3 naye akamwambia: ‘Ondoka katika nchi yako na kutoka kwa watu wako wa ukoo uje katika nchi nitakayokuonyesha.’+ 4 Ndipo akaondoka katika nchi ya Wakaldayo, akaanza kuishi Harani. Na kutoka hapo, baada ya baba yake kufa,+ Mungu akamwagiza ahamie nchi hii ambayo mnaishi sasa.+ 5 Lakini hakumpa urithi wowote ndani yake, hapana, hata sehemu ya kutosha kukanyaga kwa mguu; bali aliahidi atampa aimiliki yeye na baada yake uzao wake,*+ ingawa bado hakuwa na mtoto. 6 Isitoshe, Mungu alimwambia kwamba wazao* wake wangekuwa wageni katika nchi ambayo si yao na kwamba watu wa nchi hiyo wangewafanya kuwa watumwa na kuwatesa* kwa miaka 400.+ 7 ‘Nami nitalihukumu taifa hilo ambalo watalitumikia,’+ Mungu akasema, ‘na baada ya mambo hayo watatoka na kunitolea utumishi mtakatifu mahali hapa.’+

8 “Pia, alimpa agano la tohara,+ naye Abrahamu akawa baba ya Isaka+ na kumtahiri siku ya nane,+ na Isaka akawa baba ya* Yakobo, naye Yakobo akawa baba ya wale vichwa 12 vya familia.* 9 Na wale vichwa vya familia wakamwonea wivu Yosefu+ na kumuuza Misri.+ Lakini Mungu alikuwa pamoja naye,+ 10 akamkomboa kutoka katika dhiki zake zote, akampa kibali na hekima mbele ya Farao mfalme wa Misri. Naye Farao akamteua aongoze Misri na nyumba yake yote.+ 11 Lakini kukawa na njaa kali katika nchi yote ya Misri na Kanaani, ndiyo, dhiki kuu, na mababu zetu hawakuweza kupata chakula chochote.+ 12 Lakini Yakobo akasikia kwamba kulikuwa na chakula* huko Misri, naye akawatuma mababu zetu mara ya kwanza.+ 13 Walipoenda mara ya pili, Yosefu akajitambulisha kwa ndugu zake, naye Farao akaifahamu familia ya Yosefu.+ 14 Basi Yosefu akawatuma watu wamlete Yakobo baba yake na watu wake wote wa ukoo kutoka huko,+ jumla ya watu* 75.+ 15 Ndipo Yakobo akashuka kwenda Misri,+ naye akafa akiwa huko,+ na pia mababu zetu.+ 16 Wakabebwa mpaka Shekemu na kulazwa katika kaburi ambalo Abrahamu alikuwa amenunua kwa kiasi fulani cha fedha kutoka kwa wana wa Hamori huko Shekemu.+

17 “Wakati ulipokuwa ukikaribia wa kutimizwa kwa ahadi ambayo Mungu alikuwa amempa Abrahamu, watu wakazidi kuongezeka huko Misri, 18 mpaka alipotokea mfalme mwingine huko Misri ambaye hakumjua Yosefu.+ 19 Mfalme huyo akaitendea jamii yetu kwa hila na kuwalazimisha kimakosa akina baba wawaache watoto wao wachanga ili wafe.+ 20 Wakati huo Musa akazaliwa, naye alikuwa mwenye sura nzuri machoni pa Mungu. Akanyonyeshwa* kwa miezi mitatu nyumbani mwa baba yake.+ 21 Lakini alipoachwa,*+ binti ya Farao akamchukua na kumlea kama mwana wake mwenyewe.+ 22 Basi Musa akafundishwa hekima yote ya Wamisri. Kwa kweli, alikuwa mwenye nguvu katika maneno na matendo yake.+

23 “Sasa alipokuwa na umri wa miaka 40, wazo likaingia moyoni mwake* awatembelee * ndugu zake, wana wa Israeli.+ 24 Alipoona mmoja wao akitendewa isivyo haki, akamtetea na kulipiza kisasi kwa kumuua Mmisri. 25 Alidhani ndugu zake wangeelewa kwamba Mungu alikuwa akiwaokoa kupitia mkono wake, lakini hawakuelewa. 26 Siku iliyofuata aliwakuta wakipigana, akajaribu kuwapatanisha kwa amani, akisema: ‘Wanaume, ninyi ni ndugu. Kwa nini mnatendeana vibaya?’ 27 Lakini yule aliyekuwa akimtendea jirani yake vibaya akamsukuma Musa na kumwambia: ‘Ni nani aliyekuweka uwe mtawala na mwamuzi wetu? 28 Je, unataka kuniua kama ulivyomuua yule Mmisri jana?’ 29 Aliposikia maneno hayo, Musa akakimbia na kwenda kuishi akiwa mgeni katika nchi ya Midiani, na huko akawa baba ya wana wawili.+

30 “Baada ya miaka 40, malaika akamtokea kwenye nyika ya Mlima Sinai katika mwali wa moto wa kichaka cha miiba kilichokuwa kikiwaka.+ 31 Musa alipoona jambo hilo, akashangaa sana. Lakini alipokaribia ili kuchunguza, akasikia sauti ya Yehova* ikisema: 32 ‘Mimi ni Mungu wa mababu zako, Mungu wa Abrahamu na wa Isaka na wa Yakobo.’+ Musa akaanza kutetemeka na hakuthubutu kuchunguza zaidi. 33 Yehova* akamwambia, ‘Vua viatu vyako, kwa maana mahali unaposimama ni ardhi takatifu. 34 Hakika nimeona jinsi watu wangu walio Misri wanavyokandamizwa, nimesikia kilio chao cha huzuni,+ nami nimeshuka ili kuwaokoa. Basi njoo, nitakutuma huko Misri.’ 35 Huyo Musa ambaye walimkana wakisema: ‘Ni nani aliyekuweka uwe mtawala na mwamuzi?’+ ndiye ambaye Mungu alimtuma+ akiwa mtawala na mkombozi kupitia malaika aliyemtokea katika kichaka cha miiba. 36 Yeye ndiye aliyewaongoza watoke huko,+ akifanya mambo ya ajabu* na ishara huko Misri+ na kwenye Bahari Nyekundu+ na nyikani kwa miaka 40.+

37 “Huyo ndiye Musa aliyewaambia hivi wana wa Israeli: ‘Mungu atawainulia nabii kama mimi kutoka kati ya ndugu zenu.’+ 38 Huyo ndiye aliyekuwa kati ya kutaniko huko nyikani pamoja na malaika+ aliyezungumza naye+ kwenye Mlima Sinai na mababu zetu, naye akapokea maneno matakatifu yaliyo hai ili atupatie.+ 39 Mababu zetu walikataa kumtii, badala yake wakampuuza+ na katika mioyo yao wakarudi Misri,+ 40 wakimwambia Haruni: ‘Tutengenezee miungu itakayotuongoza. Kwa sababu hatujui lililompata huyu Musa aliyetuongoza kutoka nchi ya Misri.’+ 41 Ndipo wakatengeneza ndama siku hizo na kuiletea sanamu hiyo dhabihu nao wakaanza kufurahia kazi za mikono yao.+ 42 Basi Mungu akageuka na kuwaacha, akawakabidhi watoe utumishi mtakatifu kwa jeshi la mbinguni,+ kama vile ilivyoandikwa katika kitabu cha Manabii: ‘Enyi nyumba ya Israeli, je, mimi ndiye mliyetolea matoleo na dhabihu nyikani kwa miaka 40? 43 Bali mlilichukua hema la Moloki+ na nyota ya mungu Refani, sanamu mlizotengeneza ili kuziabudu. Kwa hiyo nitawahamishia ng’ambo ya Babiloni.’+

44 “Mababu zetu walikuwa na hema la ushahidi nyikani, lililotengenezwa kwa kufuata maagizo ambayo Mungu alimpa Musa kulingana na mfano aliokuwa amemwonyesha.+ 45 Nao mababu zetu wakalimiliki na kulileta pamoja na Yoshua kwenye nchi iliyomilikiwa na mataifa,+ ambayo Mungu aliyafukuza kutoka mbele ya mababu zetu.+ Nalo likakaa huko mpaka siku za Daudi. 46 Alipata kibali machoni pa Mungu naye akaomba pendeleo la kujenga makao kwa ajili ya Mungu wa Yakobo.+ 47 Lakini Sulemani ndiye aliyemjengea nyumba.+ 48 Hata hivyo, Aliye Juu Zaidi haishi katika nyumba zilizojengwa kwa mikono,+ kama vile nabii anavyosema: 49 ‘Mbingu ni kiti changu cha ufalme,+ nayo dunia ni kiti cha miguu yangu.+ Mtanijengea nyumba ya aina gani? Asema Yehova.* Au pako wapi mahali pangu pa kupumzikia? 50 Mkono wangu uliumba vitu hivi vyote, sivyo?’+

51 “Ninyi watu wagumu na wasiotahiriwa katika mioyo na masikio, sikuzote mnaipinga roho takatifu; kama mababu zenu walivyofanya, ndivyo mnavyofanya pia.+ 52 Ni yupi kati ya manabii ambaye mababu zenu hawakumtesa?+ Ndiyo, waliwaua wale waliotangaza mapema kuhusu kuja kwa yule mwadilifu,+ ambaye ninyi mmemsaliti na kumuua,+ 53 ninyi mliopokea Sheria kupitia malaika+ lakini hamkuishika.”

54 Basi, waliposikia mambo hayo wakawaka hasira* moyoni na kuanza kumsagia meno yao. 55 Lakini Stefano akiwa amejaa roho takatifu, akatazama mbinguni, akaona utukufu wa Mungu na wa Yesu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu,+ 56 naye akasema: “Tazama! Ninaziona mbingu zimefunguka na Mwana wa binadamu+ akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu.”+ 57 Ndipo wakapaza sauti ya juu na kuziba masikio kwa mikono yao, wote wakamrukia kwa pamoja. 58 Baada ya kumtupa nje ya jiji, wakaanza kumpiga mawe.+ Wale mashahidi+ wakaweka mavazi yao ya nje miguuni pa kijana aliyeitwa Sauli.+ 59 Walipokuwa wakimpiga mawe Stefano, akaomba hivi: “Bwana Yesu, pokea roho yangu.” 60 Kisha akapiga magoti, akasema kwa sauti kubwa: “Yehova,* usiwahesabie dhambi hii.”+ Na baada ya kusema hayo, akalala usingizi katika kifo.

8 Naye Sauli aliunga mkono kuuawa kwa Stefano.+

Kuanzia siku hiyo kutaniko lililokuwa Yerusalemu likaanza kuteswa sana; wanafunzi wote isipokuwa mitume wakatawanyika kotekote katika maeneo ya Yudea na Samaria.+ 2 Lakini wanaume waliomwogopa Mungu wakambeba Stefano ili wakamzike, nao wakamwombolezea sana. 3 Ndipo Sauli akaanza kulishambulia kutaniko. Alikuwa akivamia nyumba moja baada ya nyingine, akiwakokota nje wanaume na wanawake na kuwatupa gerezani.+

4 Hata hivyo, wale waliotawanyika wakapita katika nchi wakitangaza habari njema ya lile neno.+ 5 Sasa Filipo akashuka kwenda jiji la Samaria*+ akaanza kuwahubiria kumhusu Kristo. 6 Umati wote kwa pamoja ulikazia fikira mambo ambayo Filipo alikuwa akisema huku wakisikiliza na kutazama ishara alizokuwa akifanya. 7 Kwa maana wengi walikuwa na roho waovu, na roho hao walipaza sauti kubwa na kutoka.+ Isitoshe, wengi waliokuwa wamepooza na vilema waliponywa. 8 Basi kukawa na shangwe kubwa sana katika jiji hilo.

9 Katika jiji hilo kulikuwa na mwanamume aliyeitwa Simoni, ambaye kabla ya hapo alikuwa akifanya uchawi na kulishangaza taifa la Samaria, akidai kwamba alikuwa mtu mkuu. 10 Watu wote, kuanzia mdogo zaidi mpaka mkubwa zaidi walimkazia fikira na kusema: “Mtu huyu ndiye Nguvu za Mungu, zinazoitwa Kuu.” 11 Basi walikuwa wakimsikiliza kwa sababu alikuwa amewashangaza kwa muda fulani kwa uchawi wake. 12 Lakini walipomwamini Filipo, aliyekuwa akitangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu+ na kuhusu jina la Yesu Kristo, wanaume na pia wanawake wakabatizwa.+ 13 Simoni pia akawa mwamini na baada ya kubatizwa, akaandamana na Filipo;+ naye alishangaa kuona ishara na matendo yenye nguvu yaliyokuwa yakifanywa.

14 Mitume huko Yerusalemu waliposikia kwamba Samaria imelikubali neno la Mungu,+ wakawatuma Petro na Yohana kwao; 15 nao wakashuka kwenda huko, wakasali kwa ajili yao ili wapate roho takatifu.+ 16 Kwa maana bado haikuwa imekuja juu ya yeyote kati yao, bali walikuwa wamebatizwa tu katika jina la Bwana Yesu.+ 17 Ndipo wakaweka mikono juu yao,+ nao wakaanza kupokea roho takatifu.

18 Simoni alipoona kwamba watu walipokea roho takatifu mitume walipoweka mikono juu yao, akawatolea pesa, 19 akawaambia: “Nipeni mimi pia mamlaka hii, ili yeyote nitakayeweka mikono juu yake apokee roho takatifu.” 20 Lakini Petro akamwambia: “Fedha yako na iangamie pamoja nawe, kwa sababu ulidhani utanunua zawadi ya bure ya Mungu kwa kutumia pesa.+ 21 Wewe huna sehemu wala fungu katika jambo hili, kwa maana moyo wako si mnyoofu machoni pa Mungu. 22 Basi tubu huu ubaya wako, na umwombe Yehova* dua, ili ikiwezekana, usamehewe nia mbaya ya moyo wako; 23 kwa maana ninaona wewe ni sumu chungu* na mtumwa wa ukosefu wa uadilifu.” 24 Simoni akawaambia: “Mwombeni Yehova* dua kwa ajili yangu ili nisipatwe na lolote kati ya mambo mliyosema.”

25 Kwa hiyo, baada ya kutoa ushahidi kamili na kulisema neno la Yehova,* wakaanza kurudi Yerusalemu, nao wakaenda wakitangaza habari njema katika vijiji vingi vya Wasamaria.+

26 Hata hivyo, malaika+ wa Yehova* akamwambia Filipo: “Ondoka uende kusini kwenye barabara inayoshuka kutoka Yerusalemu kwenda Gaza.” (Hii ni barabara ya jangwani.) 27 Ndipo akaondoka na kwenda, na tazama! akamwona towashi* Mwethiopia, mwanamume aliyekuwa na mamlaka chini ya Kandake, malkia wa Waethiopia, na ambaye alisimamia hazina yote ya malkia. Alikuwa ameenda Yerusalemu kuabudu,+ 28 naye alikuwa akirudi akiwa ameketi kwenye gari lake, akimsoma kwa sauti kubwa nabii Isaya. 29 Basi roho ikamwambia Filipo: “Nenda ukaribie gari hilo.” 30 Filipo akakimbia kandokando na kumsikia akimsoma kwa sauti kubwa nabii Isaya, akamuuliza: “Je, kweli unajua* unayosoma?” 31 Akajibu: “Kwa kweli, ninawezaje kuyaelewa mtu fulani asiponiongoza?” Basi akamsihi Filipo apande aketi pamoja naye. 32 Alikuwa akisoma kifungu hiki cha Andiko: “Kama kondoo, alipelekwa machinjioni, na kama mwanakondoo aliye kimya mbele ya mtu anayemnyoa, vivyo hivyo yeye hafungui kinywa chake.+ 33 Alipokuwa akiaibishwa, hakutendewa kwa haki.+ Ni nani atakayeeleza habari za kizazi chake? Kwa sababu uhai wake unaondolewa duniani.”+

34 Ndipo yule towashi akamwambia Filipo: “Tafadhali niambie, nabii anasema hivyo kumhusu nani? Kuhusu yeye mwenyewe au mtu mwingine?” 35 Filipo akaanza kuzungumza, akianza na andiko hilo akamtangazia habari njema kumhusu Yesu. 36 Wakiwa kwenye ile barabara, wakafika mahali penye maji, na towashi akasema: “Tazama! Hapa kuna maji; ni nini kinachonizuia kubatizwa?” 37* —— 38 Ndipo akaamuru gari lisimame, na wote wawili Filipo na towashi wakaingia ndani ya maji, naye akambatiza. 39 Walipopanda kutoka ndani ya maji, roho ya Yehova* ikamwongoza Filipo upesi aondoke, na towashi hakumwona tena, bali aliendelea na safari yake akishangilia. 40 Hata hivyo, Filipo akajikuta huko Ashdodi, naye akapita katika eneo hilo, akaendelea kuyatangazia habari njema majiji yote mpaka alipofika Kaisaria.+

9 Lakini Sauli aliendelea kuwatisha wanafunzi wa Bwana akitaka kuwaua,+ basi akamwendea kuhani mkuu 2 na kumwomba barua za kwenda kwenye masinagogi huko Damasko, ili awakamate wanaume na wanawake walioifuata Ile Njia,+ na kuwaleta Yerusalemu wakiwa wamefungwa.

3 Akiwa safarini karibu kufika Damasko, ghafla nuru kutoka mbinguni ikamulika kumzunguka,+ 4 naye akaanguka chini na kusikia sauti ikimwambia: “Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa?” 5 Akauliza: “Wewe ni nani Bwana?” Akajibu: “Mimi ni Yesu,+ ambaye unamtesa.+ 6 Hata hivyo, inuka uende jijini, nawe utaambiwa unachopaswa kufanya.” 7 Wanaume waliokuwa wakisafiri pamoja naye walisimama wakiwa hawana la kusema, kwa kweli waliisikia sauti, lakini hawakumwona mtu yeyote.+ 8 Kisha Sauli akainuka, na ingawa macho yake yalikuwa yamefunguka, hangeweza kuona chochote. Basi wakamshika mkono na kumwongoza mpaka Damasko. 9 Na kwa siku tatu hakuona chochote,+ na hakula wala kunywa.

10 Huko Damasko kulikuwa na mwanafunzi aliyeitwa Anania,+ naye Bwana akamwambia katika maono: “Anania!” Akajibu: “Mimi hapa, Bwana.” 11 Bwana akamwambia: “Ondoka, uende kwenye barabara inayoitwa Nyoofu, umtafute mwanamume anayeitwa Sauli, kutoka Tarso,+ kwenye nyumba ya Yuda. Kwa maana tazama! anasali, 12 na katika maono amemwona mwanamume anayeitwa Anania akiingia na kuweka mikono juu yake ili aweze kuona tena.”+ 13 Lakini Anania akajibu: “Bwana, nimesikia kutoka kwa watu wengi kuhusu mtu huyu, jinsi alivyowatesa watakatifu wako huko Yerusalemu. 14 Na sasa amepewa mamlaka na wakuu wa makuhani ili awakamate* wote wanaoliitia jina lako.”+ 15 Lakini Bwana akamwambia: “Nenda! kwa sababu mtu huyu ni chombo nilichokichagua+ ili kupeleka jina langu kwa mataifa+ na pia kwa wafalme+ na wana wa Israeli. 16 Kwa maana nitamwonyesha waziwazi mateso mengi yatakayompata kwa sababu ya jina langu.”+

17 Basi Anania akaenda na kuingia katika ile nyumba, naye akaweka mikono yake juu ya Sauli na kusema: “Sauli, ndugu, Bwana Yesu aliyekutokea barabarani ulipokuwa ukija, amenituma ili uweze kuona tena na ujazwe roho takatifu.”+ 18 Papo hapo, vitu kama magamba vikaanguka kutoka katika macho yake, naye akaanza kuona tena. Kisha akasimama na kubatizwa, 19 naye akala chakula na kupata nguvu.

Akakaa kwa siku kadhaa pamoja na wanafunzi huko Damasko,+ 20 na mara moja akaanza kuhubiri katika masinagogi kuhusu Yesu, kwamba huyo ndiye Mwana wa Mungu. 21 Wote waliomsikia wakashangaa na kusema: “Je, huyu si yule mtu aliyewashambulia wale wanaoliitia jina hilo huko Yerusalemu?+ Je, hakuja huku ili awakamate na kuwapeleka* kwa wakuu wa makuhani?”+ 22 Lakini Sauli akazidi kupata nguvu na kuwashangaza Wayahudi walioishi Damasko, akithibitisha kupatana na akili kwamba huyu ndiye Kristo.+

23 Baada ya siku nyingi kupita, Wayahudi wakapanga njama pamoja ili kumuua.+ 24 Hata hivyo, Sauli akagundua njama yao. Pia walikuwa wakilinda malango usiku na mchana ili wamuue. 25 Basi wanafunzi wake wakamchukua na kumshusha usiku kupitia shimo ukutani, akiwa ndani ya kapu.+

26 Alipofika Yerusalemu,+ akajaribu kujiunga na wanafunzi, lakini wote walimwogopa kwa sababu hawakuamini kwamba amekuwa mwanafunzi. 27 Ndipo Barnaba+ akamsaidia na kumpeleka kwa mitume, naye akawasimulia kirefu jinsi alivyokuwa amemwona Bwana+ barabarani, na kwamba alikuwa amezungumza naye, na jinsi alivyozungumza kwa ujasiri katika jina la Yesu+ huko Damasko. 28 Basi akakaa pamoja nao, akitembea kwa uhuru* huko Yerusalemu, akizungumza kwa ujasiri katika jina la Bwana. 29 Alikuwa akiongea na kubishana na Wayahudi waliozungumza Kigiriki, lakini hao walikuwa wakijaribu kumuua.+ 30 Akina ndugu walipogundua hilo, wakampeleka Kaisaria na kumtuma aende Tarso.+

31 Ndipo kutaniko katika eneo lote la Yudea, Galilaya, na Samaria+ likaingia katika kipindi cha amani, huku likijengwa; nalo lilipokuwa likitembea katika kumwogopa Yehova* na katika faraja ya roho takatifu,+ likaendelea kuongezeka.

32 Petro alipokuwa akisafiri katika eneo hilo lote, akashuka pia kwa watakatifu walioishi Lida.+ 33 Huko akampata mwanamume aliyeitwa Ainea, ambaye alikuwa amelala kwenye kitanda chake kwa miaka minane, kwa maana alikuwa amepooza. 34 Petro akamwambia: “Ainea, Yesu Kristo anakuponya.+ Simama, utandike kitanda chako.”+ Naye akasimama mara moja. 35 Wote walioishi huko Lida na katika Nchi Tambarare ya Sharoni walipomwona, wakamgeukia Bwana.

36 Huko Yopa kulikuwa na mwanafunzi aliyeitwa Tabitha, jina ambalo linapotafsiriwa linamaanisha “Dorkasi.”* Alikuwa akitenda matendo mema na kutoa zawadi za rehema. 37 Lakini siku hizo akawa mgonjwa, akafa. Basi wakamwosha na kumlaza katika chumba cha juu. 38 Kwa kuwa Lida ilikuwa karibu na Yopa, wanafunzi waliposikia kwamba Petro alikuwa katika jiji hilo wakatuma wanaume wawili wakamsihi: “Tafadhali njoo kwetu haraka iwezekanavyo.” 39 Ndipo Petro akainuka na kwenda pamoja nao. Alipofika, wakampeleka kwenye kile chumba cha juu; nao wajane wote wakaja kwake wakilia na kuonyesha mavazi mengi na majoho* ambayo Dorkasi alikuwa ametengeneza alipokuwa pamoja nao. 40 Petro akaagiza kila mtu aende nje,+ akapiga magoti na kusali. Kisha akaugeukia ule mwili, akasema: “Tabitha, inuka!” Akafungua macho yake, na alipomwona Petro, akaketi.+ 41 Petro akamshika mkono na kumwinua, akawaita watakatifu na wajane, akamkabidhi kwao akiwa hai.+ 42 Jambo hilo likajulikana kotekote huko Yopa, na wengi wakamwamini Bwana.+ 43 Petro akakaa Yopa siku kadhaa pamoja na mtengenezaji wa ngozi aliyeitwa Simoni.+

10 Sasa huko Kaisaria kulikuwa na mwanamume aliyeitwa Kornelio, ofisa wa jeshi* wa kikosi* cha Italia. 2 Alikuwa mtu aliyemheshimu na kumwogopa Mungu, yeye pamoja na watu wote wa nyumba yake, naye aliwapa watu zawadi nyingi za rehema na aliomba dua sikuzote kwa Mungu. 3 Karibu saa tisa+ mchana* aliona waziwazi katika maono malaika wa Mungu akija na kumwita: “Kornelio!” 4 Kornelio akamkazia macho, akiwa na hofu, na kumuuliza: “Kuna nini, Bwana?” Akamwambia: “Mungu amesikia sala zako na kuona zawadi zako za rehema, naye anazikumbuka.+ 5 Basi sasa tuma watu huko Yopa wakamwite Simoni anayeitwa Petro. 6 Mtu huyo ni mgeni wa Simoni, mtengenezaji wa ngozi, aliye na nyumba kando ya bahari.” 7 Mara tu yule malaika aliyezungumza naye alipoondoka, akawaita wawili kati ya watumishi wake na mmoja wa wanajeshi wake aliyemwogopa Mungu, 8 naye akawasimulia mambo yote, kisha akawatuma waende Yopa.

9 Siku iliyofuata, wakiwa safarini karibu kufika kwenye jiji hilo, Petro alipanda kwenye paa la nyumba karibu saa sita* ili kusali. 10 Lakini akahisi njaa sana na akatamani kula. Walipokuwa wakitayarisha mlo, akapata njozi+ 11 naye akaona mbingu imefunguliwa na kitu fulani* kikishuka kama shuka kubwa la kitani, kikiteremshwa duniani kwa ncha zake nne; 12 na ndani yake mlikuwa na kila aina ya wanyama wenye miguu minne, viumbe wanaotambaa wa dunia, na ndege wa angani. 13 Kisha sauti ikamwambia: “Petro, simama, chinja ule!” 14 Lakini Petro akajibu: “Hapana Bwana, kwa maana sijawahi kula kitu chochote kilicho najisi na kisicho safi.”+ 15 Ile sauti ikamwambia mara ya pili: “Acha kuviita najisi vitu ambavyo Mungu amevitakasa.” 16 Jambo hilo likatokea mara ya tatu, na papo hapo kile chombo kikarudishwa mbinguni.

17 Petro akiwa bado anashangaa kuhusu maana ya maono hayo, wakati huohuo wale watu waliotumwa na Kornelio waliulizia nyumba ya Simoni nao walikuwa wamesimama langoni.+ 18 Nao wakaita kwa sauti na kuuliza ikiwa Simoni anayeitwa Petro alikuwa mgeni humo. 19 Petro alipokuwa akiwaza kuhusu yale maono, roho+ ikasema: “Tazama! Wanaume watatu wanakutafuta. 20 Basi simama, ushuke na kwenda pamoja nao, usiwe na shaka kamwe, kwa sababu nimewatuma.” 21 Kisha Petro akashuka kutoka ghorofani akawaambia wale wanaume: “Mimi ndiye mnayenitafuta. Kwa nini mmekuja hapa?” 22 Wakajibu: “Kornelio,+ ofisa wa jeshi, mwanamume mwadilifu anayemwogopa Mungu na mwenye sifa njema katika taifa lote la Wayahudi, alipewa maagizo na Mungu kupitia malaika mtakatifu kwamba awatume watu wakuite uje nyumbani kwake ili wasikie mambo utakayosema.” 23 Basi akawakaribisha na kukaa nao.

Siku iliyofuata Petro akaondoka pamoja nao, na baadhi ya akina ndugu wa huko Yopa wakaenda pamoja naye. 24 Kesho yake akafika Kaisaria. Bila shaka, Kornelio alikuwa akiwatarajia naye alikuwa amekusanya watu wake wa ukoo na rafiki zake wa karibu. 25 Petro alipokuwa akiingia, Kornelio akamlaki, akapiga magoti miguuni pake, na kumsujudia.* 26 Lakini Petro akamwinua, akisema: “Simama; mimi pia ni mwanadamu tu.”+ 27 Alipokuwa akizungumza naye akaingia na kuwakuta watu wengi wamekusanyika. 28 Akawaambia: “Mnajua jinsi ilivyo kinyume cha sheria kwa Myahudi kushirikiana au kumkaribia mtu wa jamii nyingine,+ lakini Mungu amenionyesha kwamba sipaswi kumwita mtu yeyote najisi au asiye safi.+ 29 Basi nilipoitwa nilikuja bila kupinga. Kwa hiyo ninawauliza: ‘Kwa nini mmeniita?’”

30 Ndipo Kornelio akasema: “Siku nne zilizopita wakati kama huu, nilikuwa nikisali katika nyumba yangu saa tisa;* wakati huohuo mwanamume aliyevaa mavazi yanayong’aa akasimama mbele yangu 31 na kusema: ‘Kornelio, sala yako imesikiwa na kukubaliwa, naye Mungu amezikumbuka zawadi zako za rehema. 32 Kwa hiyo, tuma watu waende Yopa wakamwite Simoni anayeitwa Petro. Mtu huyu ni mgeni katika nyumba ya Simoni, mtengenezaji wa ngozi, kando ya bahari.’+ 33 Mara moja nikawatuma watu kwako, nawe umefanya vizuri kuja hapa. Basi sote tupo mbele za Mungu ili kuyasikia mambo yote ambayo Yehova* amekuamuru useme.”

34 Ndipo Petro akaanza kuzungumza, akasema: “Kwa hakika ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi,+ 35 lakini katika kila taifa mtu anayemwogopa na kutenda uadilifu anakubaliwa naye.+ 36 Alituma ujumbe kwa wana wa Israeli akiwatangazia habari njema ya amani+ kupitia Yesu Kristo—huyu ndiye Bwana wa wote.+ 37 Mnajua habari iliyozungumzwa kotekote huko Yudea, kuanzia Galilaya+ baada ya ubatizo aliohubiri Yohana: 38 kumhusu Yesu aliyetoka Nazareti, jinsi Mungu alivyomtia mafuta kwa roho takatifu+ na nguvu, naye akapita katika nchi akitenda mema na kuwaponya wote waliokandamizwa na Ibilisi,+ kwa sababu Mungu alikuwa pamoja naye.+ 39 Nasi ni mashahidi wa mambo yote aliyofanya katika nchi ya Wayahudi na huko Yerusalemu; lakini walimuua kwa kumtundika kwenye mti. 40 Mungu alimfufua siku ya tatu+ na kumfunua,* 41 si kwa watu wote, bali kwa mashahidi waliochaguliwa awali na Mungu, kwetu sisi, tuliokula na kunywa pamoja naye baada ya kufufuliwa kutoka kwa wafu.+ 42 Pia, alituamuru tuwahubirie watu na kutoa ushahidi kamili+ kwamba yeye ndiye aliyeagizwa na Mungu kuwa mwamuzi wa walio hai na wafu.+ 43 Manabii wote walitoa ushahidi+ kumhusu, kwamba kila mtu anayemwamini hupokea msamaha wa dhambi kupitia jina lake.”+

44 Petro alipokuwa akizungumza kuhusu mambo hayo, roho takatifu ikaja juu ya wote waliokuwa wakisikia lile neno.+ 45 Nao waamini* waliotahiriwa ambao walikuwa wamekuja pamoja na Petro wakashangaa, kwa sababu zawadi ya bure ya roho takatifu ilikuwa ikimiminwa pia juu ya watu wa mataifa. 46 Kwa maana waliwasikia wakizungumza lugha* za kigeni na kumtukuza Mungu.+ Ndipo Petro akauliza: 47 “Je, kuna yeyote anayeweza kuwazuia hawa waliopokea roho takatifu kama tulivyoipokea wasibatizwe+ kwa maji?” 48 Ndipo akawaamuru wabatizwe katika jina la Yesu Kristo.+ Kisha wakamwomba akae pamoja nao siku kadhaa.

11 Sasa mitume na ndugu waliokuwa Yudea wakasikia kwamba watu wa mataifa pia walikuwa wamelikubali neno la Mungu. 2 Basi Petro alipopanda kwenda Yerusalemu, wale waliounga mkono kutahiriwa+ wakaanza kumkosoa,* 3 wakisema: “Uliingia ndani ya nyumba ya watu ambao hawajatahiriwa nawe ukala pamoja nao.” 4 Ndipo Petro akawafafanulia jambo hilo kwa kina, akisema:

5 “Nilipokuwa nikisali katika jiji la Yopa, niliona maono katika njozi, kitu fulani* kikishuka kama shuka kubwa la kitani, kikiteremshwa kutoka mbinguni kwa ncha zake nne, nacho kikaja moja kwa moja mpaka mahali nilipokuwa.+ 6 Nilipotazama kwa makini ndani yake, nikaona wanyama wa dunia wenye miguu minne, wanyama wa mwituni, viumbe wanaotambaa, na ndege wa angani. 7 Pia nikasikia sauti ikiniambia: ‘Petro, simama, chinja ule!’ 8 Lakini nikasema, ‘Hapana Bwana, kwa sababu kitu chochote najisi au kisicho safi hakijawahi kamwe kuingia kinywani mwangu.’ 9 Mara ya pili, ile sauti kutoka mbinguni ikajibu: ‘Wewe acha kuviita najisi vitu ambavyo Mungu amevitakasa.’ 10 Hilo likatokea mara ya tatu, na kila kitu kikavutwa juu kurudi mbinguni. 11 Wakati huohuo, wanaume watatu waliotumwa kwangu kutoka Kaisaria walikuwa wamesimama karibu na nyumba tuliyokuwa tukikaa.+ 12 Ndipo roho ikaniambia niende pamoja nao, bila kuwa na shaka hata kidogo. Lakini hawa ndugu sita pia walienda pamoja nami, nasi tukaingia ndani ya nyumba ya mwanamume huyo.

13 “Alitueleza jinsi alivyomwona malaika akiwa amesimama katika nyumba yake na kumwambia, ‘Watume watu waende Yopa wakamwite Simoni anayeitwa Petro,+ 14 naye atakuambia mambo yatayokusaidia wewe na watu wote wa nyumba yako mwokolewe.’ 15 Lakini nilipoanza kuzungumza, roho takatifu ikaja juu yao kama ilivyokuja juu yetu mwanzoni.+ 16 Ndipo nikakumbuka maneno aliyokuwa akisema Bwana: ‘Yohana alibatiza kwa maji,+ lakini ninyi mtabatizwa kwa roho takatifu.’+ 17 Kwa hiyo, ikiwa Mungu aliwapa zawadi ileile ya bure kama alivyotupatia sisi ambao tumemwamini Bwana Yesu Kristo, mimi ni nani hata niweze kumzuia* Mungu?”+

18 Waliposikia mambo hayo, wakaacha kupinga,* nao wakamtukuza Mungu wakisema: “Kwa hiyo basi, Mungu pia ameruhusu watu wa mataifa watubu ili wapate uzima.”+

19 Sasa wale waliokuwa wametawanyika+ kwa sababu ya dhiki iliyotokea kuhusiana na Stefano, wakaenda mpaka Foinike, Kipro, na Antiokia, lakini walitangaza lile neno kwa Wayahudi tu.+ 20 Hata hivyo, wanaume fulani kati yao kutoka Kipro na Kirene walikuja Antiokia na kuanza kuongea na watu waliozungumza Kigiriki, wakitangaza habari njema ya Bwana Yesu. 21 Isitoshe, mkono wa Yehova* ulikuwa pamoja nao, na idadi kubwa wakawa waamini na kumgeukia Bwana.+

22 Kutaniko lililokuwa Yerusalemu likasikia kuwahusu, nao wakamtuma Barnaba+ mpaka Antiokia. 23 Alipofika na kuziona fadhili zisizostahiliwa za Mungu, akashangilia na kuanza kuwatia moyo wote waendelee kukaa katika Bwana wakiwa wameazimia moyoni;+ 24 kwa maana alikuwa mtu mwema aliyejaa roho takatifu na imani. Na umati mkubwa ukaongezwa kwa Bwana.+ 25 Basi akaenda Tarso kumtafuta Sauli.+ 26 Baada ya kumpata, akamleta Antiokia. Basi kwa mwaka mzima wakakusanyika pamoja nao katika kutaniko na kufundisha umati mkubwa, na huko Antiokia ndiko kwa mara ya kwanza wanafunzi waliitwa Wakristo+ kupitia mwongozo wa Mungu.

27 Katika siku hizo manabii+ walishuka kutoka Yerusalemu mpaka Antiokia. 28 Mmoja wao aitwaye Agabo+ akasimama na kutabiri kupitia roho kwamba njaa kubwa ilikuwa karibu kutokea juu ya dunia yote inayokaliwa,+ na kwa kweli ilitokea wakati wa Klaudio. 29 Basi wanafunzi wakaamua kila mmoja kulingana na uwezo wake,+ watume msaada*+ kwa akina ndugu walioishi Yudea; 30 nao walifanya hivyo, wakatuma msaada kwa wazee kwa mikono ya Barnaba na Sauli.+

12 Karibu na wakati huo, Mfalme Herode akaanza kuwatesa baadhi ya watu katika kutaniko.+ 2 Alimuua kwa upanga+ Yakobo ndugu ya Yohana.+ 3 Alipoona Wayahudi wamefurahishwa na jambo hilo, akamkamata Petro pia. (Ulikuwa wakati wa Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu.)+ 4 Akamkamata na kumtia gerezani,+ chini ya ulinzi wa zamu nne za wanajeshi wanne kwa kila zamu, naye alikusudia kumtoa* mbele ya watu baada ya Pasaka. 5 Kwa hiyo, Petro alikuwa gerezani lakini kutaniko lilikuwa likisali kwa Mungu kwa bidii sana kwa ajili yake.+

6 Herode alipokuwa karibu kumtoa, usiku huo Petro alikuwa amelala akiwa amefungwa kwa minyororo miwili katikati ya wanajeshi wawili, na walinzi walikuwa mbele ya mlango wakilinda gereza. 7 Lakini tazama! malaika wa Yehova* alikuwa amesimama hapo,+ na nuru ikang’aa katika chumba cha gereza. Akamgonga Petro ubavuni, akamwamsha akisema: “Simama upesi!” Na minyororo ikaanguka kutoka kwenye mikono yake.+ 8 Malaika akamwambia: “Vaa nguo* na uvae viatu vyako.” Akafanya hivyo. Mwishowe akamwambia: “Vaa vazi lako la nje, uendelee kunifuata.” 9 Naye akatoka na kuendelea kumfuata, lakini hakujua kwamba mambo yaliyokuwa yakitendeka kupitia yule malaika yalikuwa halisi. Kwa kweli, alidhani anaona maono. 10 Wakampita mlinzi wa kwanza na wa pili, wakafika kwenye lango la chuma linaloelekea jijini, nalo likafunguka lenyewe mbele yao. Walipotoka nje wakapita kwenye barabara fulani, na mara moja yule malaika akamwacha. 11 Petro alipotambua kilichokuwa kikitendeka, akasema: “Sasa ninajua kwa hakika kwamba Yehova* alimtuma malaika wake na kunikomboa kutoka mkononi mwa Herode na mambo yote ambayo Wayahudi walitarajia.”+

12 Baada ya kutambua hivyo, akaenda kwenye nyumba ya Maria mama ya Yohana aliyeitwa Marko,+ ambamo watu wengi walikuwa wamekusanyika wakisali. 13 Alipopiga hodi kwenye mlango wa lango kuu, kijakazi anayeitwa Roda akaenda kuangalia. 14 Alipotambua sauti ya Petro, akashangilia sana hivi kwamba badala ya kufungua lango, akarudi ndani mbio na kuwaeleza kwamba Petro amesimama langoni. 15 Wakamwambia: “Umerukwa na akili.” Lakini akaendelea kusisitiza kwamba ni kweli. Wakaanza kusema: “Ni malaika wake.” 16 Lakini Petro akaendelea kubisha. Walipofungua mlango, wakamwona nao wakashangaa. 17 Lakini akawapungia mkono wanyamaze na kuwaambia kirefu jinsi Yehova* alivyomtoa gerezani, naye akasema: “Waambieni Yakobo+ na akina ndugu mambo haya.” Ndipo akatoka, akasafiri kwenda mahali pengine.

18 Basi kulipokucha, kukawa na mvurugo miongoni mwa wanajeshi kuhusu kilichompata Petro. 19 Herode akamtafuta kwa bidii, na aliposhindwa kumpata, akawahoji walinzi na kuamuru wapelekwe kuadhibiwa;+ basi akatoka Yudea na kushuka kwenda Kaisaria, akakaa huko kwa muda.

20 Sasa alikuwa amewakasirikia* watu wa Tiro na Sidoni. Basi wakaja kwake wakiwa na kusudi moja, na baada ya kumshawishi Blasto, mwanamume aliyesimamia nyumba ya mfalme,* wakatoa ombi la amani, kwa sababu nchi yao ilipata chakula kutoka kwa nchi ya mfalme. 21 Siku moja iliyochaguliwa, Herode alivaa mavazi ya kifalme akaketi kwenye kiti cha hukumu na kuanza kuwahutubia watu wote. 22 Ndipo watu waliokusanyika wakaanza kusema kwa sauti kubwa: “Hii ni sauti ya mungu, si ya mwanadamu!” 23 Papo hapo, malaika wa Yehova* akampiga, kwa sababu hakumpa Mungu utukufu, naye akaliwa na wadudu akafa.

24 Lakini neno la Yehova* likazidi kukua na kuenea.+

25 Nao Barnaba+ na Sauli, baada ya kutimiza kikamili kazi ya kutoa msaada huko Yerusalemu,+ wakarudi na kumchukua Yohana,+ ambaye pia aliitwa Marko, aende pamoja nao.

13 Basi katika kutaniko la huko Antiokia kulikuwa na manabii na walimu:+ Barnaba, Simioni aliyeitwa Nigeri, Lukio wa Kirene, Manaeni aliyeelimishwa pamoja na Herode mtawala wa wilaya, na Sauli. 2 Walipokuwa wakimhudumia* Yehova* na kufunga, roho takatifu ikasema: “Wawekeni kando kwa ajili yangu Barnaba na Sauli+ kwa kazi ambayo nimewaitia.”+ 3 Baada ya kufunga na kusali, wakaweka mikono juu yao, na kuwaacha waende.

4 Basi watu hao waliotumwa na roho takatifu, wakashuka kwenda Seleukia, na kutoka huko wakasafiri baharini kwenda Kipro. 5 Walipofika Salami, wakaanza kulitangaza neno la Mungu katika masinagogi ya Wayahudi. Pia Yohana alikuwa pamoja nao akiwahudumia.*+

6 Walipokuwa wamepita katika kisiwa chote mpaka Pafo, wakakutana na mwanamume Myahudi aliyeitwa Bar-Yesu, ambaye alikuwa mlozi na nabii wa uwongo. 7 Alikuwa pamoja na liwali* Sergio Paulo, mwanamume mwenye akili. Akawaita Barnaba na Sauli, kwa kuwa alitamani kulisikia neno la Mungu. 8 Lakini Elima mlozi (kwa maana hivyo ndivyo jina lake linavyotafsiriwa) akaanza kuwapinga, akijaribu kumzuia yule liwali asiwe mwamini. 9 Ndipo Sauli, aitwaye pia Paulo, akiwa amejaa roho takatifu, akamtazama kwa makini 10 na kumwambia: “Ewe mtu uliyejaa kila aina ya upunjaji na kila aina ya ulaghai, wewe mwana wa Ibilisi,+ wewe adui wa kila jambo la uadilifu, je, hutaacha kuzipotosha njia za Yehova* zilizo sawa? 11 Tazama! mkono wa Yehova* uko juu yako, nawe utakuwa kipofu, hutaona nuru ya jua kwa kipindi fulani.” Mara moja akaangukiwa na ukungu mzito na giza, naye akazunguka akitafuta mtu wa kumshika mkono ili amwongoze. 12 Yule liwali alipoona jambo lililotokea, akawa mwamini kwa sababu alistaajabishwa na fundisho la Yehova.*

13 Ndipo Paulo na wenzake wakasafiri baharini kutoka Pafo na kufika Perga huko Pamfilia. Lakini Yohana+ akawaacha na kurudi Yerusalemu.+ 14 Hata hivyo, wakaendelea na safari kutoka Perga hadi Antiokia huko Pisidia. Nao wakaingia ndani ya sinagogi+ siku ya Sabato, wakaketi. 15 Baada ya kusoma hadharani Sheria+ na Manabii, maofisa wasimamizi wa sinagogi wakawatuma watu kwao, wakisema: “Wanaume, akina ndugu, ikiwa mna neno lolote la kuwatia moyo watu, lisemeni.” 16 Basi Paulo akasimama, akawapungia mkono, akasema:

“Wanaume, Waisraeli nanyi wengine mnaomwogopa Mungu, sikilizeni. 17 Mungu wa watu hawa Israeli aliwachagua mababu zetu, akawainua watu hao walipokuwa wakiishi wakiwa wageni katika nchi ya Misri na kuwatoa huko kwa mkono ulioinuliwa.+ 18 Na kwa kipindi cha karibu miaka 40, akawavumilia huko nyikani.+ 19 Baada ya kuyaangamiza mataifa saba katika nchi ya Kanaani, akawapa nchi yao iwe urithi wao.+ 20 Hayo yote yalifanyika kwa karibu miaka 450.

“Baada ya hapo akawapa waamuzi hadi wakati wa nabii Samweli.+ 21 Lakini baadaye wakaomba wapewe mfalme,+ na Mungu akawapa Sauli mwana wa Kishi, mwanamume wa kabila la Benjamini,+ kwa miaka 40. 22 Baada ya kumwondoa, akamwinua Daudi awe mfalme wao,+ na akatoa ushahidi kumhusu akisema: ‘Nimempata Daudi mwana wa Yese,+ mtu anayeupendeza moyo wangu;+ atafanya mambo yote ninayotamani.’ 23 Kama alivyoahidi, kutoka katika uzao wa* mwanamume huyu, Mungu amewaletea Israeli mwokozi, yaani, Yesu.+ 24 Kabla ya huyo kufika, Yohana alikuwa amewahubiria hadharani watu wote wa Israeli wabatizwe ili kuonyesha kwamba wametubu.+ 25 Lakini Yohana alipokuwa akimalizia huduma yake, akawa akisema: ‘Mnadhani mimi ni nani? Mimi siye. Lakini tazameni! kuna Mtu anayekuja baada yangu ambaye sistahili kuvifungua viatu vya miguu yake.’+

26 “Wanaume, akina ndugu, ninyi wazao wa familia ya Abrahamu na wengine kati yenu mnaomwogopa Mungu, neno la wokovu huu limeletwa kwetu.+ 27 Kwa maana wakaaji wa Yerusalemu na watawala wao hawakumtambua huyo, lakini walipomhukumu walitimiza mambo yaliyosemwa na Manabii,+ ambayo husomwa kwa sauti kila sabato. 28 Ingawa hawakupata sababu ya kumuua,+ walimtaka Pilato aamuru auawe.+ 29 Walipokuwa wametimiza mambo yote yaliyoandikwa kumhusu, walimshusha kutoka kwenye mti na kumlaza kaburini.*+ 30 Lakini Mungu akamfufua kutoka kwa wafu,+ 31 na kwa siku nyingi akaonekana na wale waliokuwa wameenda naye kutoka Galilaya hadi Yerusalemu. Sasa hao ndio mashahidi wake kwa watu.+

32 “Basi tunawatangazia habari njema kuhusu ahadi iliyotolewa kwa mababu. 33 Mungu ameitimiza kikamili kwetu sisi, watoto wao, kwa kumfufua Yesu;+ kama ilivyoandikwa katika zaburi ya pili: ‘Wewe ni mwanangu; leo nimekuwa Baba yako.’+ 34 Na uhakika wa kwamba Yeye alimfufua kutoka kwa wafu ili asirudi tena kwenye uharibifu, Yeye ameutaja kwa njia hii: ‘Nitawaonyesha upendo mshikamanifu, ambao ni wa uaminifu,* alioahidiwa Daudi.’+ 35 Pia, zaburi nyingine inasema: ‘Hutamruhusu mshikamanifu wako aone uharibifu.’*+ 36 Kwa upande wake, Daudi alimtumikia Mungu* katika kizazi chake mwenyewe, akalala usingizi katika kifo, akazikwa pamoja na mababu zake, naye akaona uharibifu.*+ 37 Kwa upande mwingine, yule ambaye Mungu alimfufua hakuona uharibifu.*+

38 “Kwa hiyo, acheni ijulikane kwenu, akina ndugu, kwamba kupitia mtu huyo mnatangaziwa msamaha wa dhambi,+ 39 na kwamba mambo yote ambayo hamngetangazwa kuwa bila hatia kulingana na Sheria ya Musa,+ kila mtu anayeamini anatangazwa kuwa bila hatia kupitia mtu huyu.+ 40 Kwa hiyo, jihadharini ili msipatwe na mambo haya yanayosemwa katika Manabii: 41 ‘Tazameni, ninyi wenye dharau, na mshangae na kuangamia, kwa sababu ninafanya kazi fulani katika siku zenu, kazi ambayo hamtaiamini kamwe hata mtu yeyote akiwaeleza kirefu.’”+

42 Basi walipokuwa wakiondoka, watu wakawasihi wazungumzie mambo hayo Sabato iliyofuata. 43 Baada ya kusanyiko la sinagogi kumalizika, Wayahudi wengi na wageuzwa imani waliomwabudu Mungu wakawafuata Paulo na Barnaba, ambao walisema nao na kuwahimiza waendelee kubaki katika fadhili zisizostahiliwa za Mungu.+

44 Sabato iliyofuata karibu jiji lote lilikusanyika ili kulisikia neno la Yehova.* 45 Wayahudi walipouona umati, walijawa na wivu wakaanza kupinga wakikufuru mambo ambayo Paulo alikuwa akisema.+ 46 Kisha Paulo na Barnaba wakawaambia hivi kwa ujasiri: “Ilikuwa lazima neno la Mungu lihubiriwe kwenu kwanza.+ Kwa kuwa mnalikataa na kujiona hamstahili uzima wa milele, tazameni! tunawageukia mataifa.+ 47 Kwa maana Yehova* ametuamuru kwa maneno haya: ‘Nimewachagua muwe nuru ya mataifa, na muwe wokovu mpaka miisho ya dunia.’”+

48 Watu wa mataifa waliposikia jambo hilo, wakaanza kushangilia na kulitukuza neno la Yehova,* na wote waliokuwa na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele wakawa waamini. 49 Zaidi ya hayo, neno la Yehova* lilikuwa likienezwa katika nchi yote. 50 Lakini Wayahudi wakawachochea wanawake mashuhuri waliomwogopa Mungu, na wakuu wa jiji, nao wakaanza kuwatesa+ Paulo na Barnaba na kuwatupa nje ya mipaka yao. 51 Basi wakawakung’utia mavumbi yaliyokuwa kwenye miguu yao na kwenda Ikoniamu.+ 52 Nao wanafunzi wakaendelea kujawa na shangwe+ na roho takatifu.

14 Basi huko Ikoniamu wakaingia pamoja katika sinagogi la Wayahudi, wakazungumza vizuri hivi kwamba umati mkubwa wa Wayahudi na pia Wagiriki wakawa waamini. 2 Lakini Wayahudi ambao hawakuamini wakawachochea watu* wa mataifa na kuwafanya wawachukie akina ndugu.+ 3 Basi wakatumia muda mrefu wakizungumza kwa ujasiri kwa mamlaka ya Yehova,* aliyetoa ushahidi kuhusu neno la fadhili zake zisizostahiliwa kwa kuwaruhusu wafanye ishara na mambo ya ajabu.*+ 4 Hata hivyo, umati wa jiji ulikuwa umegawanyika; baadhi yao walikuwa upande wa Wayahudi lakini wengine upande wa mitume. 5 Watu wa mataifa na Wayahudi, pamoja na watawala wao walipojaribu kuwatendea kwa dharau na kuwapiga mawe,+ 6 wakajulishwa jambo hilo, nao wakakimbilia majiji ya Likaonia, Listra na Derbe, na maeneo yaliyokuwa karibu.+ 7 Wakiwa huko, wakaendelea kutangaza habari njema.

8 Huko Listra, kulikuwa na mwanamume aliyekuwa ameketi akiwa amelemaa miguu. Alikuwa kiwete tangu kuzaliwa na hakuwa ametembea kamwe. 9 Mtu huyo alikuwa akimsikiliza Paulo alipokuwa akizungumza. Paulo alipomtazama kwa makini na kuona kwamba ana imani ya kuponywa,+ 10 akasema kwa sauti kubwa: “Simama kwa miguu yako.” Ndipo yule mwanamume akaruka na kuanza kutembea.+ 11 Umati ulipoona jambo alilofanya Paulo, wakasema kwa sauti kubwa katika lugha ya Kilikaonia: “Miungu imekuwa kama wanadamu nayo imeshuka kwetu!”+ 12 Wakaanza kumwita Barnaba Zeu, naye Paulo wakamwita Herme, kwa kuwa ndiye aliyeongoza katika mazungumzo. 13 Naye kuhani wa Zeu, ambaye hekalu lake lilikuwa kwenye mwingilio wa jiji, akawaleta ng’ombe dume na mashada ya maua kwenye malango, naye alitaka kutoa dhabihu pamoja na umati.

14 Hata hivyo, mitume Barnaba na Paulo waliposikia jambo hilo, wakayararua mavazi yao na kuruka ndani ya umati wakisema kwa sauti kubwa: 15 “Wanaume, kwa nini mnafanya mambo haya? Sisi pia ni wanadamu tulio na udhaifu kama wenu.+ Nasi tunawatangazia habari njema, ili mgeuke kutoka katika mambo haya ya bure mje kwa Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo.+ 16 Katika vizazi vilivyopita aliruhusu watu wa mataifa yote waendelee kutembea katika njia zao,+ 17 ingawa hakujiacha bila ushahidi+ kwa kuwa alitenda mema, akiwapa ninyi mvua kutoka mbinguni na majira ya mavuno,+ akiwashibisha kwa chakula na kuijaza mioyo yenu furaha.”+ 18 Na ingawa walisema mambo hayo, haikuwa rahisi kwao kuuzuia umati kuwatolea dhabihu.

19 Lakini Wayahudi wakafika kutoka Antiokia na Ikoniamu wakaushawishi umati,+ nao wakampiga Paulo kwa mawe na kumkokota nje ya jiji, wakiwazia kwamba amekufa.+ 20 Hata hivyo, wanafunzi walipomzunguka, akasimama na kuingia jijini. Siku iliyofuata akaondoka pamoja na Barnaba kwenda Derbe.+ 21 Baada ya kulitangazia jiji hilo habari njema na kuwafanya watu wengi kuwa wanafunzi, wakarudi Listra, Ikoniamu, na Antiokia. 22 Wakiwa huko wakawatia nguvu wanafunzi*+ na kuwatia moyo wabaki katika imani wakisema: “Ni lazima tuingie katika Ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.”+ 23 Isitoshe, wakawaweka rasmi wazee kwa ajili yao katika kila kutaniko,+ wakatoa sala na kufunga,+ nao wakawakabidhi kwa Yehova* ambaye walikuwa wamemwamini.

24 Kisha wakapitia Pisidia wakaingia Pamfilia,+ 25 na baada ya kulitangaza neno huko Perga, wakashuka kwenda Atalia. 26 Kutoka huko wakasafiri baharini kwenda Antiokia, ambako walikuwa wamekabidhiwa kwenye fadhili zisizostahiliwa za Mungu kwa ajili ya kazi ambayo sasa walikuwa wamemaliza.+

27 Walipofika na kulikusanya kutaniko pamoja, wakawasimulia mambo mengi ambayo Mungu alikuwa amefanya kupitia kwao, na kwamba alikuwa amewafungulia mataifa mlango wa kuingia kwenye imani.+ 28 Basi wakakaa pamoja na wanafunzi kwa muda mrefu.

15 Sasa watu fulani wakashuka kutoka Yudea na kuanza kuwafundisha akina ndugu: “Msipotahiriwa kulingana na desturi ya Musa,+ hamwezi kuokolewa.” 2 Baada ya Paulo na Barnaba kutoelewana na kubishana sana na watu hao, wakapanga Paulo na Barnaba na wengine wapande kwenda kwa mitume na wazee huko Yerusalemu+ kuuliza kuhusu jambo* hilo.

3 Basi, baada ya kusindikizwa umbali fulani na kutaniko, watu hao wakaenda wakapitia Foinike na Samaria, wakisimulia kirefu kuhusu kugeuka kwa watu wa mataifa, nao wakafanya akina ndugu washangilie sana. 4 Walipofika Yerusalemu, walikaribishwa kwa fadhili na kutaniko na mitume na wazee, nao wakawasimulia mambo mengi ambayo Mungu alifanya kupitia kwao. 5 Lakini baadhi ya wale wa madhehebu ya Mafarisayo ambao sasa walikuwa waamini wakasimama kutoka kwenye viti vyao na kusema: “Ni lazima watahiriwe na kuwaamuru washike Sheria ya Musa.”+

6 Basi, mitume na wazee wakakusanyika pamoja ili kulichunguza jambo hilo. 7 Baada ya kujadiliana sana,* Petro akasimama na kuwaambia: “Wanaume, akina ndugu, mnajua vema kwamba tangu siku za zamani Mungu alinichagua kati yenu ili kupitia kinywa changu watu wa mataifa wasikie neno la habari njema na kuamini.+ 8 Pia, Mungu anayeujua moyo,+ alitoa ushahidi kwa kuwapa roho takatifu,+ kama vile alivyotupatia sisi. 9 Naye hakutofautisha hata kidogo kati yetu na wao,+ bali aliisafisha mioyo yao kwa imani.+ 10 Basi kwa nini sasa mnamjaribu Mungu kwa kuweka kwenye shingo za wanafunzi nira+ ambayo mababu zetu na sisi wenyewe tulishindwa kuibeba?+ 11 Badala yake, sisi tunaamini kwamba tunaokolewa kupitia fadhili zisizostahiliwa za Bwana Yesu+ katika njia ileile wanayookolewa.”+

12 Ndipo kikundi chote kikanyamaza na kuanza kuwasikiliza Barnaba na Paulo wakisimulia ishara nyingi na mambo ya ajabu* ambayo Mungu alifanya kupitia kwao miongoni mwa mataifa. 13 Walipomaliza kuzungumza, Yakobo akasema: “Wanaume, akina ndugu, nisikilizeni. 14 Simioni+ amesimulia kikamili jinsi Mungu kwa mara ya kwanza alivyoelekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake.+ 15 Na maneno ya Manabii yanaunga mkono jambo hilo, kama ilivyoandikwa: 16 ‘Baada ya mambo hayo nitarudi na kuliinua tena hema la* Daudi ambalo limeanguka chini; nitayajenga upya magofu yake na kulirudisha tena, 17 ili watu wanaobaki wamtafute Yehova* kwa bidii, pamoja na watu wa mataifa yote, watu wanaoitwa kwa jina langu, asema Yehova,* anayefanya mambo haya,+ 18 yanayojulikana tangu zamani.’+ 19 Kwa hiyo uamuzi wangu* ni kutowataabisha watu wa mataifa wanaomgeukia Mungu,+ 20 bali kuwaandikia wajiepushe na vitu vilivyochafuliwa na sanamu,+ na uasherati,*+ na vitu vilivyonyongwa,* na damu.+ 21 Kwa maana tangu nyakati za kale kuna watu ambao wamekuwa wakihubiri kumhusu Musa katika kila jiji, kwa sababu yeye husomwa kwa sauti kubwa katika masinagogi kila sabato.”+

22 Ndipo mitume na wazee, pamoja na kutaniko lote wakaamua kuwatuma wanaume waliochaguliwa kutoka miongoni mwao waende Antiokia pamoja na Paulo na Barnaba; waliwatuma Yuda aliyeitwa Barsaba, na Sila,+ wanaume waliokuwa wakiongoza kati ya akina ndugu. 23 Wakaandika maneno haya na kuyatuma kupitia kwao:

“Mitume na wazee, ndugu zenu, kwa ndugu walio huko Antiokia,+ Siria, na Kilikia ambao ni wa kutoka kwa mataifa: Salamu! 24 Kwa kuwa tumesikia kwamba watu fulani walitoka miongoni mwenu na kuwataabisha kwa mambo waliyosema,+ wakijaribu kuwavuruga,* ingawa hatukuwapa maagizo yoyote, 25 tumefikia kauli moja kwamba tuwachague wanaume ili tuwatume kwenu pamoja na wapendwa wetu Barnaba na Paulo, 26 wanaume ambao wametoa uhai wao* kwa ajili ya jina la Bwana wetu Yesu Kristo.+ 27 Kwa hiyo, tunawatuma Yuda na Sila, ili wao pia waeleze mambo hayohayo kwa maneno.+ 28 Kwa maana roho takatifu+ na sisi wenyewe tumeona ni vizuri tusiwaongezee ninyi mzigo zaidi ila mambo haya ya lazima: 29 kuendelea kujiepusha na vitu vilivyotolewa dhabihu kwa sanamu,+ na damu,+ na vitu vilivyonyongwa,*+ na uasherati.*+ Mkijiepusha kwa uangalifu na mambo haya, mtafanikiwa. Afya njema kwenu!”*

30 Basi, watu hao walipoondoka wakashuka kwenda Antiokia, nao wakakusanya kundi lote pamoja na kuwapa barua hiyo. 31 Baada ya kuisoma, wakashangilia kwa sababu ya kutiwa moyo. 32 Nao Yuda na Sila, kwa sababu walikuwa manabii pia, wakawatia moyo akina ndugu kwa hotuba nyingi na kuwaimarisha.+ 33 Baada ya kukaa huko kwa muda fulani, ndugu hao wakawaacha warudi kwa amani kwa wale waliokuwa wamewatuma. 34* —— 35 Lakini Paulo na Barnaba wakakaa Antiokia, wakifundisha na kutangaza habari njema ya neno la Yehova,* wakiwa pamoja na wengine wengi.

36 Baada ya siku kadhaa, Paulo akamwambia Barnaba: “Turudi* tukawatembelee akina ndugu katika kila jiji ambalo tulitangaza neno la Yehova* tuone jinsi wanavyoendelea.”+ 37 Barnaba alikuwa ameazimia kwenda na Yohana, aliyeitwa Marko.+ 38 Lakini Paulo hakutaka waende pamoja naye, kwa sababu alikuwa amewaacha huko Pamfilia na hakuenda pamoja nao kwenye kazi.+ 39 Ndipo wakagombana kwa ukali hivi kwamba wakaachana; naye Barnaba+ akamchukua Marko na kusafiri pamoja naye baharini kwenda Kipro. 40 Paulo akamchagua Sila na kuondoka baada ya akina ndugu kumkabidhi kwenye fadhili zisizostahiliwa za Yehova.*+ 41 Akapitia Siria na Kilikia, akiyaimarisha makutaniko.

16 Kwa hiyo akafika Derbe na pia Listra.+ Huko kulikuwa na mwanafunzi aliyeitwa Timotheo,+ mama yake alikuwa Myahudi aliyekuwa mwamini, lakini baba yake alikuwa Mgiriki, 2 na alishuhudiwa vema na akina ndugu huko Listra na Ikoniamu. 3 Paulo alitamani Timotheo aende pamoja naye, basi akamchukua na kumtahiri kwa sababu ya Wayahudi waliokuwa katika sehemu hizo,+ kwa maana wote walijua kwamba baba yake ni Mgiriki. 4 Walipokuwa wakipita katika majiji, walikuwa wakiwapa maagizo yaliyokuwa yameamuliwa na mitume na wazee waliokuwa Yerusalemu ili wayashike.+ 5 Ndipo kwa kweli makutaniko yakaendelea kuimarishwa katika imani na kuongezeka idadi siku baada ya siku.

6 Zaidi ya hayo, wakapitia Frigia na nchi ya Galatia,+ kwa sababu roho takatifu iliwakataza kuhubiri lile neno katika mkoa wa Asia. 7 Vilevile, walipofika Misia wakajaribu kuingia Bithinia,+ lakini roho ya Yesu haikuwaruhusu. 8 Basi wakapita* Misia na kushuka mpaka Troa. 9 Naye Paulo akaona maono usiku—mwanamume Mmakedonia alikuwa amesimama hapo akimsihi: “Vuka uingie Makedonia utusaidie.” 10 Mara tu alipoona maono hayo, tukajaribu kuingia Makedonia, tukikata kauli kwamba Mungu alikuwa ametuita tuwatangazie habari njema.

11 Basi tukatoka Troa na kusafiri moja kwa moja baharini hadi Samothrake, lakini kesho yake tukafika Neapoli; 12 na kutoka huko tukaenda Filipi,+ koloni ambalo ni jiji kuu la wilaya ya Makedonia. Tukakaa katika jiji hilo siku kadhaa. 13 Siku ya Sabato tukatoka nje ya lango kando ya mto, ambako tulifikiri kuna mahali pa sala, tukaketi na kuanza kuzungumza na wanawake waliokuwa wamekusanyika. 14 Na mwanamke aliyeitwa Lidia, muuzaji wa nguo za rangi ya zambarau, wa jiji la Thiatira+ aliyekuwa mwabudu wa Mungu, alikuwa akisikiliza, na Yehova* akaufungua moyo wake wazi ili asikilize kwa makini mambo ambayo Paulo alikuwa akisema. 15 Basi yeye na watu wa nyumbani mwake walipobatizwa,+ akatusihi: “Ikiwa mmeniona kuwa mwaminifu kwa Yehova,* njooni mkae nyumbani kwangu.” Naye akatuhimiza sana twende.

16 Ikatukia kwamba tulipokuwa tukienda mahali pale pa kusali, tulikutana na kijakazi fulani mwenye roho, roho mwovu wa uaguzi.+ Aliwapatia mabwana zake faida nyingi kwa kubashiri.* 17 Msichana huyo alikuwa akimfuata Paulo na sisi akisema kwa sauti kubwa: “Watu hawa ni watumwa wa Mungu Aliye Juu Zaidi+ nao wanawatangazia ninyi njia ya wokovu.” 18 Akaendelea kufanya hivyo kwa siku nyingi. Mwishowe Paulo akachoshwa, akageuka na kumwambia huyo roho: “Ninakuamuru katika jina la Yesu Kristo umtoke.” Naye akatoka saa hiyohiyo.+

19 Basi, mabwana zake walipoona kwamba wamepoteza tumaini lao la kupata faida,+ wakawakamata Paulo na Sila wakawakokota hadi sokoni kwa watawala.+ 20 Wakawapeleka kwa mahakimu wa raia, na kusema: “Watu hawa wanasumbua sana jiji letu.+ Wao ni Wayahudi, 21 nao wanatangaza desturi ambazo si halali kwetu kuzikubali au kuzifuata, kwa kuwa sisi ni Waroma.” 22 Umati ukasimama pamoja dhidi yao, nao wale mahakimu wa raia, baada ya kuyararua mavazi yao, wakaamuru wapigwe kwa fimbo.+ 23 Baada ya kuwapiga sana, wakawatupa gerezani na kumwagiza mlinzi wa jela awalinde.+ 24 Kwa sababu alipewa agizo hilo, akawatupa katika gereza la ndani zaidi na kuifunga miguu yao katika mikatale.

25 Lakini karibu katikati ya usiku, Paulo na Sila walikuwa wakisali na kumsifu Mungu kwa wimbo,+ nao wafungwa walikuwa wakiwasikiliza. 26 Ghafla tetemeko kubwa la ardhi likatokea na misingi ya jela ikatikiswa. Isitoshe, milango yote ikafunguliwa mara moja, na vifungo vyao wote vikafunguka.+ 27 Mlinzi wa jela alipoamka na kuona milango ya gereza imefunguka, akauchomoa upanga wake naye karibu ajiue, akidhani wafungwa walikuwa wametoroka.+ 28 Lakini Paulo akamwambia kwa sauti kubwa: “Usijiumize, kwa maana sisi sote tupo hapa!” 29 Kwa hiyo akaomba taa akakimbia ndani, akitetemeka, akaanguka chini mbele ya Paulo na Sila. 30 Akawaleta nje na kusema: “Mabwana zangu, nifanye nini ili niokolewe?” 31 Wakajibu: “Mwamini Bwana Yesu, nawe utaokolewa, wewe na watu wa nyumba yako.”+ 32 Nao wakamhubiria neno la Yehova* yeye pamoja na wote waliokuwa katika nyumba yake. 33 Naye akawachukua saa hiyo ya usiku, akaosha vidonda vyao. Kisha yeye na watu wote wa nyumba yake wakabatizwa bila kukawia.+ 34 Akawaleta nyumbani kwake akaandaa meza mbele yao, naye akashangilia sana pamoja na watu wote wa nyumba yake kwa kuwa sasa alikuwa amemwamini Mungu.

35 Ilipofika mchana, mahakimu wa raia wakawatuma maofisa wa polisi wakaseme: “Wafungueni wale watu.” 36 Mlinzi wa jela akamweleza Paulo maneno yao: “Mahakimu wa raia wamewatuma watu ili ninyi wawili mfunguliwe. Basi tokeni sasa mwende zenu kwa amani.” 37 Lakini Paulo akawaambia: “Walitupiga viboko hadharani bila kutuhukumu,* ingawa sisi ni Waroma,+ na wakatutupa gerezani. Je, sasa wanatufukuza kwa siri? Hapana, haiwezekani! Acha waje watutoe nje wao wenyewe.” 38 Wale maofisa wa polisi wakawaeleza mahakimu wa raia maneno hayo. Nao wakaogopa waliposikia kwamba watu hao walikuwa Waroma.+ 39 Basi wakaja na kuwasihi na baada ya kuwatoa nje, wakawaomba waondoke katika jiji hilo. 40 Lakini wakatoka gerezani na kwenda nyumbani kwa Lidia; na walipowaona akina ndugu, wakawatia moyo+ kisha wakaondoka.

17 Sasa wakasafiri kupitia Amfipoli na Apolonia wakaenda hadi Thesalonike,+ ambako kulikuwa na sinagogi la Wayahudi. 2 Basi kulingana na desturi ya Paulo+ akaingia ndani ya sinagogi, na kwa sabato tatu akajadiliana nao akitumia Maandiko,+ 3 akieleza na kuthibitisha kwa marejeo kwamba ilikuwa lazima Kristo ateseke+ na kufufuliwa kutoka kwa wafu,+ akisema: “Huyu ndiye Kristo, Yesu huyu ninayewatangazia ninyi.” 4 Kwa hiyo, baadhi yao wakaamini na kujiunga na Paulo na Sila,+ pia umati mkubwa wa Wagiriki waliomwabudu Mungu, vilevile wanawake wengi mashuhuri.

5 Lakini Wayahudi wakawa na wivu,+ wakakusanya wanaume fulani waovu waliokuwa wakizurura sokoni, wakafanyiza kikundi chenye ghasia kisha wakazusha fujo jijini. Wakaishambulia nyumba ya Yasoni wakitaka Paulo na Sila waletwe nje kwenye kile kikundi. 6 Walipowakosa wakamkokota Yasoni na baadhi ya akina ndugu mpaka kwa watawala wa jiji, wakisema kwa sauti kubwa: “Watu hawa ambao wameipindua* dunia inayokaliwa wako hapa pia,+ 7 naye Yasoni amewakaribisha. Watu hao wote wanapinga maagizo ya Kaisari, wakisema kuna mfalme mwingine, Yesu.”+ 8 Ule umati na watawala wa jiji waliposikia mambo hayo, wakashtuka; 9 baada ya kuchukua dhamana ya kutosha kutoka kwa Yasoni na wale wengine, wakawaacha waende zao.

10 Mara tu ilipofika usiku, akina ndugu wakawatuma Paulo na Sila waende Beroya. Walipofika huko, wakaingia ndani ya sinagogi la Wayahudi. 11 Sasa watu hawa walikuwa wasikivu kuliko wale wa Thesalonike, kwa maana walilikubali neno kwa hamu kubwa ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo. 12 Kwa hiyo wengi wao wakawa waamini, vilevile wanawake wengi Wagiriki walioheshimiwa na pia baadhi ya wanaume. 13 Lakini Wayahudi kutoka Thesalonike waliposikia kwamba Paulo alikuwa akitangaza pia neno la Mungu huko Beroya, wakaja huko ili kuchochea na kuuvuruga umati.+ 14 Mara moja akina ndugu wakamsindikiza Paulo mpaka baharini,+ lakini Sila na Timotheo wakabaki huko. 15 Hata hivyo, wale waliomsindikiza Paulo wakaenda naye mpaka Athene, kisha wakarudi baada ya kupokea maagizo kwamba Sila na Timotheo+ wamfuate Paulo haraka iwezekanavyo.

16 Paulo alipokuwa akiwasubiri huko Athene, roho yake ikaudhika sana alipoona kwamba jiji hilo lilikuwa limejaa sanamu. 17 Basi akaanza kujadiliana katika sinagogi pamoja na Wayahudi na watu wengine waliomwabudu Mungu na kila siku pamoja na watu aliowakuta sokoni. 18 Lakini baadhi ya Waepikurea na wanafalsafa Wastoa wakaanza kubishana naye, wengine wao wakisema: “Mpigadomo huyu anataka kusema nini?” Nao wengine: “Inaonekana anatangaza miungu ya kigeni.” Kwa sababu alikuwa akihubiri habari njema ya Yesu na ufufuo.+ 19 Kwa hiyo wakamshika na kumpeleka Areopago, wakisema: “Je, tunaweza kujua ni fundisho gani hili jipya unalozungumzia? 20 Kwa maana unaanzisha mambo yaliyo mageni masikioni mwetu, na tunataka kujua yanamaanisha nini.” 21 Kwa kweli, Waathene wote na wageni waliokaa* huko walitumia muda wao wa starehe bila kufanya kitu kingine isipokuwa kuambiana au kusikiliza jambo jipya. 22 Basi Paulo akasimama katikati ya Areopago+ na kusema:

“Wanaume wa Athene, ninaona kwamba katika mambo yote mnaonekana kuwa mnaogopa sana miungu* kuliko watu wengine.+ 23 Kwa mfano, nilipokuwa nikipita na kutazama kwa uangalifu vitu vyenu vya ibada, niliona pia madhabahu iliyoandikwa, ‘Kwa Mungu Asiyejulikana.’ Kwa hiyo, kile mnachoabudu bila kujua, hicho ndicho ninachowatangazia. 24 Mungu aliyeumba ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, akiwa, kama alivyo, Bwana wa mbingu na dunia,+ hakai katika mahekalu yaliyotengenezwa kwa mikono;+ 25 wala hatumikiwi kwa mikono ya binadamu kana kwamba anahitaji kitu chochote,+ kwa sababu yeye mwenyewe huwapa watu wote uhai na pumzi+ na vitu vyote. 26 Naye alifanyiza kila taifa la watu kutoka kwa mtu mmoja+ ili wakae juu ya uso wa dunia nzima,+ na akaamuru nyakati na kuweka mipaka ya makao ya watu,+ 27 ili wamtafute Mungu, ikiwa watapapasa-papasa wakimtafuta na kwa kweli wampate,+ ingawa, kwa hakika, hayuko mbali na kila mmoja wetu. 28 Kwa maana kupitia kwake tuko hai, tunatembea, na tunaishi, hata kama vile ambavyo baadhi ya washairi wenu wamesema, ‘Kwa maana sisi pia ni watoto* wake.’

29 “Kwa hiyo, kwa kuwa sisi ni watoto* wa Mungu,+ hatupaswi kufikiri kwamba Mungu ni kama dhahabu au fedha au jiwe, kama kitu kilichochongwa kwa ufundi na ubunifu wa wanadamu.+ 30 Ni kweli, Mungu ameachilia nyakati hizo za kutojua;+ lakini sasa anawatangazia wanadamu wote kila mahali kwamba wanapaswa kutubu. 31 Kwa sababu ameweka siku ambayo anakusudia kuihukumu+ kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia mwanamume ambaye amemweka rasmi, naye ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua kutoka kwa wafu.”+

32 Sasa waliposikia kuhusu ufufuo wa wafu, baadhi yao wakaanza kumdhihaki,+ huku wengine wakisema: “Tutakusikiliza kuhusu jambo hili wakati mwingine.” 33 Basi Paulo akawaacha, 34 lakini wanaume fulani wakajiunga naye na kuwa waamini. Miongoni mwao kulikuwa na Dionisio, aliyekuwa mwamuzi wa mahakama ya Areopago, na mwanamke aliyeitwa Damari, na wengineo.

18 Baada ya hayo, akatoka Athene na kwenda Korintho. 2 Naye akamkuta Myahudi aliyeitwa Akila,+ mzaliwa wa Ponto aliyekuwa amekuja hivi karibuni kutoka Italia na Prisila mke wake, kwa sababu Klaudio alikuwa ameagiza Wayahudi wote waondoke Roma. Basi akaenda kwao, 3 na kwa sababu walifanya kazi ileile, akakaa nyumbani kwao na kufanya kazi pamoja nao,+ kwa maana kazi yao ilikuwa ya kutengeneza mahema. 4 Alikuwa akitoa hotuba* katika sinagogi+ kila sabato+ na kuwashawishi Wayahudi na Wagiriki.

5 Basi, Sila+ na Timotheo+ waliposhuka kutoka Makedonia, Paulo akaanza kushughulika sana na lile neno, akiwatolea Wayahudi ushahidi ili kuthibitisha kwamba Yesu ndiye Kristo.+ 6 Lakini walipoendelea kumpinga na kumtukana, akayakung’uta mavazi yake+ na kuwaambia: “Damu yenu na iwe juu ya vichwa vyenu wenyewe.+ Mimi ni safi.+ Kuanzia sasa nitaenda kwa watu wa mataifa.”+ 7 Basi akatoka humo* na kuingia katika nyumba ya mwanamume aliyeitwa Titio Yusto, mwabudu wa Mungu, ambaye nyumba yake ilikuwa imeshikana na sinagogi. 8 Lakini Krispo,+ ofisa msimamizi wa sinagogi akamwamini Bwana, yeye pamoja na watu wote wa nyumba yake. Na Wakorintho wengi waliosikia wakaanza kuamini na kubatizwa. 9 Isitoshe, Bwana akamwambia Paulo katika maono usiku: “Usiogope, bali endelea kusema na usinyamaze, 10 kwa sababu niko pamoja nawe+ na hakuna mtu atakayekushambulia ili kukudhuru; kwa maana nina watu wengi katika jiji hili.” 11 Basi akakaa huko kwa mwaka mmoja na miezi sita, akifundisha neno la Mungu kati yao.

12 Galio alipokuwa liwali* wa Akaya, Wayahudi wakaungana, wakamshambulia Paulo na kumpeleka kwenye kiti cha hukumu, 13 wakisema: “Mtu huyu anawashawishi watu wamwabudu Mungu kwa njia iliyo kinyume cha sheria.” 14 Lakini Paulo alipokuwa karibu kuzungumza, Galio akawaambia Wayahudi: “Enyi Wayahudi, kama kweli lingekuwa kosa fulani au uhalifu mkubwa, ningekuwa na sababu ya kuwasikiliza kwa subira. 15 Lakini kama mnabishania maneno na majina na sheria yenu,+ amueni wenyewe. Mimi sitaki kuwa mwamuzi wa mambo hayo.” 16 Ndipo akawafukuza kutoka mbele ya kiti cha hukumu. 17 Basi wote wakamkamata Sosthene,+ ofisa msimamizi wa sinagogi na kuanza kumpiga mbele ya kiti cha hukumu. Lakini Galio hakujihusisha kamwe na mambo hayo.

18 Hata hivyo, baada ya kukaa siku kadhaa, Paulo aliwaaga akina ndugu naye akasafiri baharini kwenda Siria, pamoja na Prisila na Akila. Alikuwa amekata nywele zake huko Kenkrea,+ kwa sababu alikuwa ameweka nadhiri. 19 Basi wakafika Efeso, akawaacha huko; lakini yeye akaingia ndani ya sinagogi na kujadiliana na Wayahudi.+ 20 Ingawa waliendelea kumsihi akae kwa muda mrefu zaidi, hakukubali 21 bali aliwaaga na kuwaambia: “Nitarudi kwenu tena, Yehova* akipenda.” Naye akasafiri baharini kutoka Efeso 22 na kushuka mpaka Kaisaria. Akapanda kwenda na kulisalimia kutaniko,* kisha akashuka kwenda Antiokia.+

23 Baada ya kukaa huko kwa muda fulani, akaondoka na kwenda sehemu mbalimbali katika nchi ya Galatia na Frigia,+ akiwaimarisha wanafunzi wote.+

24 Sasa Myahudi aliyeitwa Apolo,+ mzaliwa wa Aleksandria akafika Efeso; alikuwa mwanamume mwenye ufasaha na ujuzi mwingi wa Maandiko. 25 Mwanamume huyu alikuwa amefundishwa* njia ya Yehova,* na akiwa amewaka roho, alikuwa akizungumza na kufundisha kwa usahihi kumhusu Yesu, lakini alifahamu ubatizo wa Yohana tu. 26 Akaanza kuzungumza kwa ujasiri katika sinagogi, nao Prisila na Akila+ walipomsikia, wakamchukua na kumfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu. 27 Pia, kwa sababu alitaka kuvuka kwenda Akaya, akina ndugu wakawaandikia wanafunzi wakiwahimiza wamkaribishe kwa fadhili. Basi alipofika huko, akawasaidia sana wale ambao kupitia fadhili zisizostahiliwa za Mungu walikuwa wameamini; 28 kwa maana alithibitisha kikamili hadharani na kwa juhudi nyingi kwamba Wayahudi walikuwa wamekosea, na kuwaonyesha kwa Maandiko kuwa Yesu ndiye Kristo.+

19 Apolo+ alipokuwa Korintho, Paulo alipita bara na kushuka mpaka Efeso.+ Aliwakuta wanafunzi fulani huko 2 akawauliza: “Mlipoanza kuamini, je, mlipokea roho takatifu?”+ Wakamjibu: “Hata hatujasikia kwamba kuna roho takatifu.” 3 Basi akawauliza: “Mlibatizwa katika nini?” Wakajibu: “Katika ubatizo wa Yohana.”+ 4 Paulo akasema: “Yohana aliwabatiza watu ili kuonyesha kwamba wametubu,+ akiwaambia wamwamini yule ambaye angekuja baada yake,+ yaani, Yesu.” 5 Waliposikia hivyo, wakabatizwa katika jina la Bwana Yesu. 6 Paulo alipoweka mikono juu yao, wakapokea roho takatifu,+ nao wakaanza kuzungumza kwa lugha za kigeni na kutoa unabii.+ 7 Wote walikuwa wanaume karibu 12.

8 Akaingia katika sinagogi,+ na kwa miezi mitatu akazungumza kwa ujasiri, akitoa hotuba na kujadiliana kwa ushawishi kuhusu Ufalme wa Mungu.+ 9 Lakini baadhi yao wakawa wagumu* na wakakataa kuamini, huku wakizungumza vibaya kuhusu Ile Njia+ mbele ya umati. Basi akawaacha+ na kuwatenga wanafunzi kutoka kwao, na kila siku alikuwa akitoa hotuba katika ukumbi wa shule ya Tirano. 10 Aliendelea kufanya hivyo kwa miaka miwili, hivi kwamba wote walioishi katika mkoa wa Asia wakasikia neno la Bwana, Wayahudi na Wagiriki pia.

11 Na Mungu akaendelea kufanya matendo yenye nguvu yasiyo ya kawaida kupitia mikono ya Paulo,+ 12 hivi kwamba hata nguo na vitambaa vilivyogusa mwili wake vilipelekewa wagonjwa,+ nao wakaponywa magonjwa, na roho waovu wakatoka.+ 13 Lakini baadhi ya Wayahudi waliosafiri huku na huku wakifukuza roho waovu wakajaribu pia kutumia jina la Bwana Yesu kwa wale waliokuwa na roho waovu; wakisema: “Ninakuamuru kwa jina la Yesu ambaye Paulo humhubiri.”+ 14 Wana saba wa Skewa, mkuu wa makuhani wa Kiyahudi, walikuwa wakifanya hivyo. 15 Lakini yule roho mwovu akawaambia: “Ninamjua Yesu+ nami ninamfahamu Paulo;+ lakini ninyi ni nani?” 16 Ndipo mtu huyo aliyekuwa na roho mwovu akawarukia, akawazidi nguvu mmoja baada ya mwingine na kuwashinda, hivi kwamba wakatoka mbio katika nyumba hiyo wakiwa uchi na wakiwa wameumizwa. 17 Watu wote wakajua jambo hilo, Wayahudi na Wagiriki walioishi huko Efeso; na wote wakaogopa, nalo jina la Bwana Yesu likaendelea kutukuzwa. 18 Na wengi kati ya wale waliokuwa waamini walikuwa wakija na kuungama, wakieleza waziwazi kuhusu mazoea yao. 19 Kwa kweli, idadi kubwa ya wale waliozoea kufanya uchawi wakakusanya vitabu vyao pamoja na kuviteketeza mbele ya kila mtu.+ Nao wakafanya hesabu na kupata vitabu hivyo vilikuwa na thamani ya vipande 50,000 vya fedha. 20 Hivyo kwa njia yenye nguvu, neno la Yehova* likazidi kukua na kusitawi.+

21 Baada ya mambo hayo kutukia, Paulo akaazimia katika roho yake kwamba baada ya kupitia Makedonia+ na Akaya, atasafiri kwenda Yerusalemu.+ Akasema: “Baada ya kwenda huko, lazima pia nione Roma.”+ 22 Basi akawatuma wawili kati ya wale waliomhudumia, Timotheo+ na Erasto,+ waende Makedonia lakini yeye akakaa kwa muda fulani katika mkoa wa Asia.

23 Wakati huo kukatokea mvurugo+ mkubwa kuhusu Ile Njia.+ 24 Kwa maana mtu fulani aliyeitwa Demetrio, fundi wa fedha aliyetengeneza vihekalu vya fedha vya Artemi, aliwaletea mafundi faida kubwa.+ 25 Akawakusanya pamoja na wengine waliofanya kazi kama hiyo na kuwaambia: “Wanaume, mnajua vema kwamba tunapata mafanikio yetu kutokana na biashara hii. 26 Sasa mnaona na kusikia kwamba si katika Efeso tu,+ bali pia katika karibu mkoa wote wa Asia, Paulo huyu ameushawishi umati mkubwa na kuwafanya wawe na maoni tofauti, akisema kwamba miungu iliyotengenezwa kwa mikono, kwa kweli si miungu.+ 27 Isitoshe, kuna hatari kwamba biashara yetu itapata sifa mbaya na pia hekalu la Artemi mungu mkuu wa kike litaonwa kuwa si kitu, naye anayeabudiwa katika mkoa wote wa Asia na dunia inayokaliwa atakosa utukufu.” 28 Waliposikia jambo hilo wakajawa na hasira, nao wakaanza kusema kwa sauti kubwa: “Artemi wa Waefeso ni mkuu!”

29 Basi jiji likajaa mvurugo na wote pamoja wakakimbia na kuingia katika ukumbi wa maonyesho, wakiwakokota Gayo na Aristarko,+ Wamakedonia waliokuwa wakisafiri pamoja na Paulo. 30 Naye Paulo alitaka kuingia walimokuwa watu hao, lakini wanafunzi hawakumruhusu. 31 Hata baadhi ya wasimamizi wa sherehe na michezo waliomtendea kwa urafiki, wakamtumia ujumbe wakimsihi asijihatarishe kwa kuingia katika ukumbi wa maonyesho. 32 Kwa kweli, baadhi yao walikuwa wakisema kwa sauti kubwa jambo moja na wengine jambo tofauti; kwa maana kusanyiko hilo lilikuwa limevurugika, na wengi wao hawakujua kwa nini walikuwa wamekusanyika. 33 Basi wakamtoa Aleksanda kwenye umati, huku Wayahudi wakimsukuma mbele, naye Aleksanda akapunga mkono akitaka kujitetea mbele ya watu. 34 Lakini walipotambua kwamba alikuwa Myahudi, wote wakaanza kupaza sauti kwa pamoja kwa karibu saa mbili wakisema: “Artemi wa Waefeso ni mkuu!”

35 Mwishowe, karani wa jiji akaunyamazisha umati, kisha akasema: “Watu wa Efeso, kwa kweli ni nani kati ya wanadamu ambaye hajui kwamba jiji la Efeso ndilo mlinzi wa hekalu la Artemi mkuu na sanamu iliyoanguka kutoka mbinguni? 36 Kwa kuwa mambo haya hayawezi kukanushwa, tulieni na msitende haraka haraka. 37 Kwa maana mmewaleta hapa watu hawa ambao hawaibi katika mahekalu wala kumkufuru mungu wetu wa kike. 38 Basi ikiwa Demetrio+ na mafundi walio pamoja naye wana kesi dhidi ya mtu fulani, siku za mahakama hufanywa na kuna maliwali;* wanaweza kushtakiana huko. 39 Lakini ikiwa mnatafuta jambo lingine zaidi ya hilo, linapaswa kuamuliwa katika kusanyiko la kawaida. 40 Kwa kweli tunakabili hatari ya kushtakiwa kwa uchochezi kuhusu tukio la leo, kwa sababu hatuna msingi wa kuwa na kikundi hiki chenye machafuko.” 41 Baada ya kusema mambo hayo, akauagiza umati utawanyike.

20 Baada ya ghasia kutulia, Paulo akatuma watu wawaite wanafunzi, akawatia moyo na kuwaaga, kisha akaanza safari yake ya kwenda Makedonia. 2 Baada ya kupitia maeneo hayo na kuwatia moyo kwa maneno mengi wale waliokuwa huko, akafika Ugiriki. 3 Akakaa huko miezi mitatu, lakini kwa sababu Wayahudi walikuwa wametunga hila dhidi yake+ alipokuwa karibu kusafiri kwenda Siria, akaamua kurudi kupitia Makedonia. 4 Alienda pamoja na Sopatro mwana wa Piro wa Beroya, Aristarko+ na Sekundo wa Wathesalonike, Gayo wa Derbe, Timotheo+ na, kutoka wilaya ya Asia, Tikiko+ na Trofimo.+ 5 Wanaume hao wakatangulia na kutusubiri huko Troa; 6 lakini sisi tukaanza kusafiri baharini kutoka Filipi baada ya Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu,+ siku tano baadaye tukawafikia huko Troa, tukakaa huko siku saba.

7 Siku ya kwanza ya juma, tulipokuwa tumekusanyika ili kupata mlo, Paulo akaanza kuwahutubia, kwa sababu angeondoka kesho yake; naye akarefusha hotuba yake mpaka katikati ya usiku. 8 Basi kulikuwa na taa nyingi katika chumba cha juu tulimokuwa tumekusanyika. 9 Kijana aitwaye Eutiko alikuwa ameketi dirishani, naye akalala usingizi mzito Paulo alipokuwa akiongea, basi akalemewa na usingizi, akaanguka chini kutoka ghorofa ya tatu, akaokotwa akiwa amekufa. 10 Lakini Paulo akashuka kutoka ghorofani, akajitupa juu yake akamkumbatia+ na kusema: “Acheni kupiga kelele, kwa maana yuko hai.”*+ 11 Kisha akapanda ghorofani, akaanzisha mlo* na kula chakula. Akaendelea kuzungumza kwa muda mrefu, mpaka mapambazuko, kisha akaondoka. 12 Basi wakamchukua mvulana huyo akiwa hai, wakafarijika sana.

13 Sasa tukaenda kwenye meli na kusafiri mpaka Aso, ambako tulikusudia kumchukua Paulo, kwa maana baada ya kutuagiza hivyo, alikusudia kwenda huko kwa miguu. 14 Basi alipotufikia huko Aso, akapanda kwenye meli tulimokuwa, tukaenda Mitilene. 15 Tukaondoka huko kesho yake, tukafika karibu na Kio, lakini siku ya pili tukafika Samo, na siku iliyofuata tukafika Mileto. 16 Paulo alikuwa ameamua kuendelea na safari bila kupitia Efeso,+ ili asitumie muda wowote katika mkoa wa Asia, kwa maana alikuwa akiharakisha kufika Yerusalemu+ siku ya Sherehe ya Pentekoste kama ingewezekana.

17 Hata hivyo, kutoka Mileto akatuma watu kwenda Efeso wawaite wazee wa kutaniko hilo waje. 18 Walipokuja akawaambia: “Mnajua vema jinsi nilivyotenda kati yenu tangu siku ya kwanza niliyokanyaga mkoa wa Asia,+ 19 nilivyomtumikia Bwana kwa unyenyekevu wote*+ na machozi na majaribu yaliyonipata kupitia hila za Wayahudi, 20 nami sikuepuka kuwaambia ninyi jambo lolote lenye faida* na kuwafundisha hadharani+ na nyumba kwa nyumba.+ 21 Lakini nilitoa ushahidi kikamili kwa Wayahudi na Wagiriki kuhusu toba+ kwa Mungu na kuwa na imani katika Bwana wetu Yesu.+ 22 Na sasa, tazameni! nikiwa nimefungwa katika* roho, ninasafiri kwenda Yerusalemu, ingawa sijui mambo yatakayonipata huko, 23 isipokuwa kutoka jiji mpaka jiji roho takatifu inanitolea ushahidi tena na tena, ikisema kwamba nitafungwa gerezani na kupatwa na dhiki.+ 24 Hata hivyo, sioni uhai wangu* kuwa muhimu kwangu,* mradi tu nimalize mwendo wangu+ na huduma niliyopokea kutoka kwa Bwana Yesu, kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu.

25 “Na sasa, tazameni! ninajua kwamba hakuna yeyote kati yenu ninyi niliowahubiria kuhusu Ufalme atakayeona uso wangu tena. 26 Basi ninawaita ili mshuhudie leo hii kwamba mimi sina hatia ya damu ya mtu yeyote,+ 27 kwa maana sikukosa kuwaambia mashauri yote ya* Mungu.+ 28 Jiangalieni wenyewe+ na kundi lote, ambalo kati yake roho takatifu imewaweka ninyi rasmi muwe waangalizi,+ mlichunge kutaniko la Mungu,+ ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.+ 29 Ninajua kwamba nitakapoondoka mbwamwitu wenye kukandamiza wataingia miongoni mwenu+ nao hawatalitendea kundi kwa wororo, 30 na kutoka miongoni mwenu watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.+

31 “Kwa hiyo endeleeni kukesha, na kukumbuka kwamba kwa miaka mitatu,+ usiku na mchana, sikuacha kumwonya kila mmoja wenu kwa machozi. 32 Na sasa ninawakabidhi ninyi kwa Mungu na kwa neno la fadhili zake zisizostahiliwa, ambalo linaweza kuwajenga na kuwapa urithi kati ya wale wote waliotakaswa.+ 33 Sikutamani fedha, dhahabu, wala mavazi ya mtu yeyote.+ 34 Ninyi wenyewe mnajua kwamba nimefanya kazi kwa hii mikono yangu ili kupata mahitaji yangu+ na ya wale walio pamoja nami. 35 Nimewaonyesha ninyi katika mambo yote kwamba kwa kufanya kazi kwa bidii hivyo,+ ni lazima mwasaidie walio dhaifu, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, aliposema: ‘Kuna furaha zaidi katika kutoa+ kuliko ilivyo katika kupokea.’”

36 Baada ya kusema mambo haya, akapiga magoti pamoja nao wote na kusali. 37 Kwa kweli, wote wakalia sana, nao wakamkumbatia Paulo* na kumbusu kwa upendo,* 38 kwa maana waliumia sana aliposema kwamba hawangeuona uso wake tena.+ Kisha wakamsindikiza mpaka kwenye meli.

21 Tulipofaulu kuachana nao na kusafiri baharini, tulienda moja kwa moja mpaka Kosi, siku iliyofuata tukafika Rode, na kutoka huko tukaenda Patara. 2 Tulipopata meli iliyokuwa ikivuka kwenda Foinike, tukapanda na kuondoka. 3 Baada ya kufika mahali tulipoweza kuona kisiwa cha Kipro, tukakiacha upande wa kushoto tukasafiri mpaka Siria, tukafika Tiro ambako meli ilipaswa kushusha shehena. 4 Tukawatafuta wanafunzi na tulipowapata tukakaa huko siku saba. Lakini kupitia roho, wakamwambia Paulo tena na tena asikanyage Yerusalemu.+ 5 Baada ya muda wetu huko kwisha, tukaondoka na kuanza safari, lakini wote kutia ndani wanawake na watoto, wakatusindikiza mpaka nje ya jiji. Tukapiga magoti ufuoni, tukasali, 6 kisha tukaagana. Tukapanda meli, nao wakarudi nyumbani kwao.

7 Ndipo tukakamilisha safari ya baharini kutoka Tiro tukafika Tolemai, tukawasalimu akina ndugu na kukaa nao siku moja. 8 Siku iliyofuata tukaondoka na kufika Kaisaria, tukaingia katika nyumba ya Filipo mweneza-injili, aliyekuwa mmoja wa wale wanaume saba,+ nasi tukakaa pamoja naye. 9 Mtu huyo alikuwa na binti wanne ambao hawakuwa wameolewa,* nao walitoa unabii.+ 10 Lakini baada ya kukaa huko kwa siku kadhaa, nabii aliyeitwa Agabo+ akashuka kutoka Yudea. 11 Akaja mahali tulipokuwa akachukua mshipi wa Paulo, akajifunga miguu na mikono na kusema: “Hivi ndivyo roho takatifu inavyosema, ‘Wayahudi kule Yerusalemu watamfunga+ hivi mwanamume ambaye mshipi huu ni wake, nao watamtia mikononi mwa watu wa mataifa.’”+ 12 Tuliposikia hayo, sisi na wale waliokuwa hapo tukaanza kumsihi Paulo asipande kwenda Yerusalemu. 13 Kisha Paulo akasema: “Kwa nini mnalia na kujaribu kunivunja moyo?* Muwe na hakika kwamba niko tayari si kufungwa tu bali pia kufa huko Yerusalemu kwa ajili ya jina la Bwana Yesu.”+ 14 Tuliposhindwa kumshawishi, tukaacha kumkataza,* tukasema: “Mapenzi ya Yehova* na yatendeke.”

15 Sasa baada ya siku hizo tukajitayarisha kwa ajili ya safari kisha tukaanza kuelekea Yerusalemu. 16 Baadhi ya wanafunzi kutoka Kaisaria wakaenda pamoja nasi, wakatupeleka kwa Mnasoni wa Kipro, mwanafunzi wa zamani ambaye tulipaswa kuwa wageni nyumbani kwake. 17 Tulipofika Yerusalemu, akina ndugu wakatukaribisha kwa furaha. 18 Lakini siku iliyofuata Paulo akaingia pamoja nasi kwa Yakobo,+ na wazee wote walikuwapo. 19 Akawasalimu na kuanza kusimulia kirefu mambo ambayo Mungu alifanya miongoni mwa mataifa kupitia huduma yake.

20 Baada ya kusikia jambo hilo, wakaanza kumtukuza Mungu, lakini wakamwambia: “Ndugu, unaona jinsi ambavyo maelfu ya Wayahudi wamekuwa waamini, na wote wanafuata Sheria kwa bidii.+ 21 Lakini wamesikia uvumi kukuhusu kwamba umekuwa ukiwafundisha Wayahudi wote kati ya mataifa kuiasi sheria ya Musa, ukiwaambia wasiwatahiri watoto wao wala kufuata desturi zilizowekwa.+ 22 Sasa tufanye nini? Kwa kweli watasikia kwamba umefika. 23 Basi fanya jambo tunalokuambia: Tuna wanaume wanne waliojiwekea nadhiri. 24 Nenda pamoja na watu hawa ukajitakase kisherehe pamoja nao na kuwagharimia, ili wanyolewe vichwa vyao. Ndipo kila mtu atajua kwamba uvumi walioambiwa kukuhusu si wa kweli, bali unatembea kwa utaratibu, na pia unashika Sheria.+ 25 Kuhusu waamini kutoka kati ya mataifa, tumewatumia uamuzi wetu kwa maandishi kwamba wanapaswa kuepuka vitu vilivyotolewa dhabihu kwa sanamu+ na pia damu,+ na vitu vilivyonyongwa,*+ na uasherati.”*+

26 Ndipo Paulo akaenda pamoja na wanaume hao siku iliyofuata, akajitakasa kisherehe pamoja nao,+ naye akaingia hekaluni ili kutoa taarifa kuhusu wakati ambapo siku za kujitakasa zingekwisha na toleo litolewe kwa ajili ya kila mmoja wao.

27 Sasa zile siku saba zilipokaribia kwisha, Wayahudi kutoka Asia walipomwona hekaluni, wakauchochea umati wote, nao wakamkamata, 28 wakisema kwa sauti kubwa: “Wanaume wa Israeli, tusaidieni! Huyu ndiye mwanamume anayewafundisha watu kila mahali dhidi ya watu wetu na Sheria yetu na mahali hapa. Isitoshe, hata aliwaingiza Wagiriki hekaluni naye amepatia unajisi mahali hapa patakatifu.”+ 29 Kwa maana mwanzoni walikuwa wamemwona Trofimo+ Mwefeso jijini akiwa pamoja naye, nao wakadhani Paulo alikuwa amemwingiza hekaluni. 30 Jiji lote likawa na machafuko, watu wakakimbia pamoja wakamkamata Paulo na kumkokota nje ya hekalu, na mara moja milango ikafungwa. 31 Walipokuwa wakijaribu kumuua, kamanda wa kikosi cha jeshi akapata habari kwamba Yerusalemu yote ilikuwa na vurugu; 32 mara moja akachukua wanajeshi na maofisa wa jeshi wakakimbia kwenda huko. Walipomwona kamanda wa jeshi na wanajeshi, wakaacha kumpiga Paulo.

33 Ndipo yule kamanda wa jeshi akakaribia akamweka chini ya ulinzi na kuamuru afungwe kwa minyororo miwili;+ kisha akauliza huyo ni nani na alikuwa amefanya nini. 34 Lakini baadhi ya watu katika umati wakaanza kusema jambo moja kwa sauti kubwa na wengine jambo tofauti. Basi aliposhindwa kujua jambo lolote la hakika kwa sababu ya fujo hizo, akaamuru aletwe kwenye makao ya wanajeshi. 35 Lakini alipofika kwenye ngazi, alilazimika kubebwa na wanajeshi kwa sababu umati ulitaka kumuumiza, 36 kwa maana umati wa watu uliendelea kuwafuata, ukisema kwa sauti kubwa: “Auawe!”

37 Alipokuwa karibu kuingizwa katika makao ya wanajeshi, Paulo akamuuliza yule kamanda wa jeshi: “Je, ninaruhusiwa kukuambia jambo fulani?” Naye akamuuliza: “Je, unajua kuzungumza Kigiriki? 38 Kwani wewe si yule Mmisri ambaye hivi majuzi alianzisha uchochezi na kuwaongoza wale wanaume 4,000 wenye visu hadi nyikani?” 39 Paulo akamjibu: “Mimi kwa kweli ni Myahudi,+ wa Tarso+ huko Kilikia, raia wa jiji maarufu. Basi nakuomba uniruhusu nizungumze na watu hawa.” 40 Baada ya kupewa ruhusa, Paulo, akiwa amesimama kwenye ngazi, akawapungia watu mkono. Waliponyamaza kabisa, akawahutubia kwa lugha ya Kiebrania,+ akisema:

22 “Wanaume, akina ndugu na akina baba, nisikilizeni ninapojitetea mbele yenu sasa.”+ 2 Basi, waliposikia anazungumza nao kwa lugha ya Kiebrania, wakazidi kukaa kimya, naye akasema: 3 “Mimi ni Myahudi,+ aliyezaliwa huko Tarso ya Kilikia,+ nilielimishwa katika jiji hili miguuni pa Gamalieli,+ na kufundishwa kwa usahihi kabisa Sheria ya mababu,+ nikiwa na bidii kwa ajili ya Mungu kama nyote mlivyo leo.+ 4 Niliitesa Njia hii kufikia kifo, nikiwafunga na kuwatia magerezani wanaume na wanawake pia,+ 5 kama vile kuhani mkuu na kusanyiko lote la wazee wanavyoweza kutoa ushahidi. Nilipata pia barua kutoka kwao ili nizipeleke kwa akina ndugu huko Damasko, nami nilikuwa ninaenda kuwakamata wale waliokuwa huko na kuwaleta Yerusalemu wakiwa wamefungwa ili waadhibiwe.

6 “Lakini nilipokuwa safarini nikikaribia kufika Damasko, karibu katikati ya mchana, ghafla nuru kubwa kutoka mbinguni ikamulika kunizunguka,+ 7 nami nikaanguka chini na kusikia sauti ikiniuliza: ‘Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa?’ 8 Nikajibu: ‘Wewe ni nani Bwana?’ Naye akaniambia: ‘Mimi ni Yesu Mnazareti, ambaye unamtesa.’ 9 Basi watu waliokuwa pamoja nami, waliiona ile nuru lakini hawakuisikia sauti ya yule aliyezungumza nami. 10 Ndipo nikamuuliza: ‘Nifanye nini Bwana?’ Bwana akaniambia: ‘Simama, uende Damasko, na huko utaambiwa kila kitu ambacho umepangiwa kufanya.’+ 11 Lakini kwa kuwa sikuweza kuona chochote kwa sababu ya utukufu wa nuru hiyo, wale waliokuwa pamoja nami wakanishika mkono na kuniongoza mpaka Damasko.

12 “Kisha mwanamume anayeitwa Anania, aliyemwogopa Mungu kulingana na Sheria, na kushuhudiwa vema na Wayahudi wote walioishi huko, 13 akaja nilipokuwa. Akasimama kando yangu, akaniambia, ‘Sauli ndugu, anza kuona tena!’ Papo hapo nikatazama juu nikamwona.+ 14 Akasema: ‘Mungu wa mababu zetu amekuchagua ujue mapenzi yake na umwone yule aliye mwadilifu+ na kuisikia sauti ya kinywa chake, 15 kwa sababu utakuwa shahidi wake kwa watu wote kuhusu mambo ambayo umeona na kusikia.+ 16 Na sasa kwa nini unakawia? Simama, ubatizwe na uoshe dhambi zako+ kwa kuliitia jina lake.’+

17 “Lakini niliporudi Yerusalemu,+ nikiwa ninasali hekaluni, nikapata njozi 18 na kumwona Bwana akiniambia: ‘Fanya upesi uondoke Yerusalemu haraka, kwa sababu hawatakubali ushahidi wako kunihusu.’+ 19 Nami nikasema: ‘Bwana, wao wenyewe wanajua vema kwamba nilikuwa nikiwatia gerezani na kuwapiga viboko katika sinagogi moja baada ya lingine wale waliokuamini;+ 20 na damu ya Stefano shahidi wako ilipokuwa ikimwagwa, nilikuwa nimesimama kando na kukubaliana na jambo hilo nikiyalinda mavazi ya nje ya wale waliokuwa wakimuua.’+ 21 Na bado akaniambia: ‘Nenda kwa sababu nitakutuma kwa mataifa yaliyo mbali.’”+

22 Basi wakaendelea kumsikiliza mpaka aliposema maneno hayo. Kisha wakasema kwa sauti kubwa: “Mwondoeni duniani mtu kama huyu, hafai kuishi!” 23 Kwa sababu walikuwa wakipiga kelele na kutupa mavazi yao ya nje huku na huku na kurusha mavumbi hewani,+ 24 yule kamanda wa jeshi akaagiza Paulo aingizwe katika makao ya wanajeshi na kuamuru ahojiwe huku akipigwa mijeledi, ili ajue kwa nini hasa walikuwa wakimpigia Paulo kelele hivyo. 25 Lakini walipokuwa wamemnyoosha ili kumpiga mijeledi, Paulo akamuuliza ofisa wa jeshi aliyekuwa amesimama hapo: “Je, ni halali kwenu kumpiga mijeledi Mroma* ambaye hajahukumiwa?”*+ 26 Yule ofisa wa jeshi aliposikia hivyo, akaenda kwa kamanda wa jeshi na kumwambia: “Unakusudia kufanya nini? Kwa maana mtu huyu ni Mroma.” 27 Basi kamanda wa jeshi akakaribia na kumuuliza: “Niambie, wewe ni Mroma?” Akajibu: “Ndiyo.” 28 Kamanda wa jeshi akasema: “Mimi nilinunua haki hizo za kuwa raia kwa pesa nyingi.” Paulo akasema: “Lakini mimi nina haki hizo kwa kuzaliwa.”+

29 Kwa hiyo, mara moja watu waliokuwa karibu kumhoji kwa kumtesa wakamwacha; na kamanda wa jeshi akaogopa alipotambua kwamba Paulo ni Mroma na kwamba alikuwa amemfunga kwa minyororo.+

30 Basi siku iliyofuata, kwa kuwa alitaka kujua hasa sababu iliyowafanya Wayahudi wamshtaki, akamfungua na kuwaamuru wakuu wa makuhani na Sanhedrini yote wakusanyike. Kisha akamleta Paulo chini na kumsimamisha kati yao.+

23 Paulo akaikazia macho Sanhedrini, akasema: “Wanaume, akina ndugu, nimetenda kwa dhamiri safi kabisa+ mbele za Mungu mpaka leo hii.” 2 Ndipo kuhani mkuu Anania akawaagiza wale waliosimama kando yake wampige kofi mdomoni. 3 Paulo akamwambia: “Mungu atakupiga wewe, ewe ukuta uliopakwa chokaa. Je, unaketi kunihukumu kulingana na Sheria na wakati uleule unaivunja Sheria hiyo kwa kuamuru nipigwe?” 4 Wale waliosimama kando wakamuuliza: “Je, unamtukana kuhani mkuu wa Mungu?” 5 Paulo akasema: “Akina ndugu, sikujua yeye ni kuhani mkuu. Kwa maana imeandikwa, ‘Usiseme vibaya kuhusu mtawala wa watu wako.’”+

6 Sasa Paulo, akijua kwamba sehemu moja ilikuwa Masadukayo na nyingine Mafarisayo, akasema kwa sauti kubwa katika Sanhedrini: “Wanaume, akina ndugu, mimi ni Farisayo,+ mwana wa Mafarisayo. Ninahukumiwa kwa sababu ya tumaini la ufufuo wa wafu.” 7 Baada ya kusema hivyo, kukatokea mtengano kati ya Mafarisayo na Masadukayo, na kusanyiko likagawanyika. 8 Kwa maana Masadukayo husema hakuna ufufuo wala malaika wala roho, lakini Mafarisayo huyakubali* hayo yote.+ 9 Basi kukawa na vurugu, na baadhi ya waandishi wa chama cha Mafarisayo wakasimama na kuanza kubishana kwa ukali, wakisema: “Hatuoni kosa lolote katika mtu huyu, lakini ikiwa roho au malaika alizungumza naye+—.” 10 Basi mzozo ulipozidi kuongezeka, kamanda wa jeshi akaogopa kwamba watamrarua-rarua Paulo, akaamuru wanajeshi washuke wamnyakue kutoka kati yao kisha wamlete kwenye makao ya wanajeshi.

11 Lakini usiku uliofuata Bwana akasimama kando yake na kumwambia: “Jipe moyo!+ Kwa maana kama vile ambavyo umekuwa ukitoa ushahidi kamili kunihusu katika Yerusalemu, ndivyo utakavyotoa ushahidi huko Roma pia.”+

12 Ilipofika mchana, Wayahudi wakafanya hila na kujifunga kwa kiapo cha laana, wakisema hawatakula wala kunywa mpaka watakapomuua Paulo. 13 Kulikuwa na watu zaidi ya 40 waliofanya hila hiyo iliyofungwa kwa kiapo. 14 Watu hao wakaenda kwa wakuu wa makuhani na wazee na kusema: “Tumejifunga kabisa kwa laana* kwamba hatutakula chochote mpaka tutakapomuua Paulo. 15 Basi ninyi pamoja na Sanhedrini mwambieni kamanda wa jeshi amshushe kwenu kana kwamba mnataka kuchunguza zaidi kesi yake. Lakini kabla hajafika, tutakuwa tayari kumuua.”

16 Hata hivyo, mwana wa dada ya Paulo akasikia kuhusu mpango wao wa kumvizia, akaingia kwenye makao ya wanajeshi na kumjulisha Paulo. 17 Kisha Paulo akamwita mmoja wa maofisa wa jeshi na kumwambia: “Mpeleke kijana huyu kwa kamanda wa jeshi, kwa maana ana jambo la kumweleza.” 18 Basi akampeleka kwa kamanda wa jeshi na kusema: “Mfungwa Paulo aliniita na kuniomba nimlete kijana huyu kwako, kwa sababu ana jambo la kukuambia.” 19 Kamanda wa jeshi akamshika mkono akampeleka faraghani na kumuuliza: “Unataka kuniambia nini?” 20 Akasema: “Wayahudi wamekubaliana kukuomba umshushe Paulo kwenye Sanhedrini kesho, kana kwamba wanataka kupata habari zaidi kuhusu kesi yake.+ 21 Lakini usikubali wakushawishi, kwa maana kuna wanaume zaidi ya 40 kati yao walio tayari kumvizia, nao wamejifunga kwa laana* kwamba hawatakula wala kunywa mpaka watakapomuua;+ na sasa wako tayari, wakisubiri ruhusa kutoka kwako.” 22 Basi yule kamanda wa jeshi akamwacha kijana huyo aende baada ya kumwagiza: “Usimwambie mtu yeyote kwamba umenijulisha jambo hili.”

23 Akawaita maofisa wawili wa jeshi na kuwaambia: “Wekeni tayari wanajeshi 200 waende moja kwa moja mpaka Kaisaria, pia wapanda farasi 70 na watu 200 wenye mikuki, saa tatu usiku.⁠ 24 Pia, andaeni farasi kwa ajili ya Paulo ili asafiri salama mpaka kwa gavana Feliksi.” 25 Naye akaandika barua yenye ujumbe huu:

26 “Klaudio Lisia kwa Mtukufu, Gavana Feliksi: Salamu! 27 Mwanamume huyu alikamatwa na Wayahudi nao walikuwa karibu kumuua, lakini nikaja haraka pamoja na wanajeshi wangu na kumwokoa,+ baada ya kujua kwamba ni Mroma.+ 28 Nilitaka kujua kwa nini walikuwa wakimshtaki, basi nikampeleka kwenye Sanhedrini yao.+ 29 Nikatambua kwamba ameshtakiwa kuhusu maswali ya Sheria yao,+ lakini hajashtakiwa kwa jambo lolote linalostahili kifo au kufungwa gerezani. 30 Lakini kwa sababu nimejulishwa njama iliyopangwa dhidi ya mwanamume huyu,+ ninamtuma kwako mara moja, na kuwaamuru wale wanaomshtaki wamshtaki mbele yako.”

31 Basi wale wanajeshi wakamchukua Paulo+ usiku kama walivyoagizwa wakamleta mpaka Antipatri. 32 Siku iliyofuata wakawaruhusu wapanda farasi waende pamoja naye, nao wakarudi kwenye makao ya wanajeshi. 33 Wale wapanda farasi wakaingia Kaisaria, wakamkabidhi gavana ile barua na kumleta Paulo mbele yake. 34 Basi akaisoma na kuuliza ametoka mkoa gani, akajua kwamba alikuwa ametoka Kilikia.+ 35 Akasema: “Nitasikiliza kesi yako kwa makini wale wanaokushtaki watakapofika.”+ Naye akaamuru awekwe chini ya ulinzi katika jumba la kifalme la Herode.

24 Siku tano baadaye kuhani mkuu Anania+ akashuka pamoja na baadhi ya wazee na msemaji wa hadharani* aliyeitwa Tertulo, nao wakawasilisha kesi yao dhidi ya Paulo mbele ya gavana.+ 2 Alipoitwa, Tertulo akaanza kumshtaki, akisema:

“Kwa kuwa tunafurahia amani nyingi kupitia kwako, na kwa busara yako mabadiliko yanatokea katika taifa hili, 3 nyakati zote na kila mahali tunatambua jambo hilo kwa shukrani nyingi sana, ewe Mtukufu Feliksi. 4 Lakini ili nisitumie muda wako mwingi, ninakuomba kwa fadhili zako utusikilize kwa ufupi. 5 Kwa maana tumemwona mtu huyu kuwa msumbufu,*+ akichochea uasi+ miongoni mwa Wayahudi wote katika dunia yote inayokaliwa, naye ni kiongozi wa madhehebu ya Wanazareti.+ 6 Pia alijaribu kulichafua hekalu, basi tukamkamata.+ 7* —— 8 Wewe mwenyewe utakapomhoji, utagundua mambo haya yote ambayo tunamshtaki.”

9 Ndipo Wayahudi pia wakajiunga katika shambulio hilo, wakisisitiza kwamba mambo hayo ni ya kweli. 10 Gavana alipomtolea Paulo ishara ili azungumze, akajibu:

“Ninajua vema kwamba umekuwa mwamuzi wa taifa hili kwa miaka mingi, nami nafurahi kujitetea mbele yako.+ 11 Unaweza kujihakikishia kwamba hazijapita zaidi ya siku 12 tangu nilipopanda kwenda kuabudu huko Yerusalemu;+ 12 nao hawakunipata hekaluni nikibishana na mtu yeyote wala kuchochea kikundi chenye ghasia, katika masinagogi au kotekote jijini. 13 Wala hawawezi kukuthibitishia mambo wanayonishtaki sasa hivi. 14 Lakini ninakiri jambo hili kwako, kwamba kulingana na njia wanayoiita ‘madhehebu,’ hivyo ndivyo ninavyomtolea utumishi mtakatifu Mungu wa mababu zangu,+ kwa kuwa ninaamini mambo yote yaliyo katika Sheria na yaliyoandikwa katika Manabii.+ 15 Nami nina tumaini kwa Mungu, tumaini ambalo watu hawa pia wanatazamia, kwamba kutakuwa na ufufuo+ wa waadilifu na wasio waadilifu pia.+ 16 Kwa sababu hiyo sikuzote ninajitahidi kudumisha dhamiri safi* mbele za Mungu na wanadamu.+ 17 Sasa baada ya miaka kadhaa, nilirudi ili kuleta zawadi za rehema+ kwa taifa langu na kutoa matoleo. 18 Nilipokuwa nikishughulikia mambo hayo, walinikuta hekaluni nikiwa nimetakaswa kisherehe,+ lakini sikuwa na umati wala sikuwa ninasababisha fujo. Lakini kulikuwa na Wayahudi fulani kutoka mkoa wa Asia 19 ambao wanapaswa kuwa hapa mbele yako ili wanishtaki ikiwa kwa kweli wana jambo lolote dhidi yangu.+ 20 Au uwaambie watu walio hapa waseme wenyewe kosa walilopata nilipokuwa nimesimama mbele ya Sanhedrini, 21 isipokuwa jambo hili moja nililosema kwa sauti kubwa nilipokuwa nimesimama kati yao: ‘Mimi ninahukumiwa leo mbele yenu kwa sababu ya ufufuo wa wafu!’”+

22 Hata hivyo, Feliksi, akiwa anajua vizuri ukweli kuhusu Njia hii,+ akaahirisha kesi yao kwa kusema: “Lisia kamanda wa jeshi atakapokuja, nitaamua mambo haya yanayowahusu.” 23 Naye akamwagiza ofisa wa jeshi kwamba mtu huyo awekwe chini ya kizuizi lakini apewe uhuru fulani, na watu wake waruhusiwe kumhudumia.

24 Siku kadhaa baadaye Feliksi akaja na Drusila mke wake, aliyekuwa Myahudi, akawatuma watu wamwite Paulo naye akamsikiliza akizungumza kuhusu imani katika Kristo Yesu.+ 25 Lakini Paulo alipokuwa akiongea kuhusu uadilifu na kujizuia* na hukumu itakayokuja,+ Feliksi akaogopa na kumwambia: “Kwa sasa unaweza kwenda, lakini nitakapopata nafasi nitakuita tena.” 26 Wakati huohuo alitumaini kwamba Paulo angempa pesa. Kwa hiyo, akamwita mara nyingi na kuzungumza naye. 27 Lakini miaka miwili ilipokwisha, Porkio Festo alichukua nafasi ya Feliksi; na kwa sababu Feliksi alitamani kukubaliwa na Wayahudi,+ akamwacha Paulo akiwa amefungwa.

25 Kwa hiyo, baada ya Festo+ kufika katika mkoa na kuchukua mamlaka, siku tatu baadaye alipanda kwenda Yerusalemu kutoka Kaisaria. 2 Nao wakuu wa makuhani na watu mashuhuri kati ya Wayahudi wakamweleza mashtaka dhidi ya Paulo.+ Basi wakaanza kumwomba Festo 3 awaonyeshe kibali* kwa kumwita Paulo aje Yerusalemu. Lakini walikuwa wanapanga kumvizia Paulo na kumuua barabarani.+ 4 Hata hivyo, Festo akajibu kwamba Paulo alipaswa kuzuiliwa huko Kaisaria na kwamba baada ya muda mfupi yeye mwenyewe angerudi huko. 5 Akasema: “Basi wale walio na mamlaka kati yenu washuke pamoja nami na kumshtaki, ikiwa kwa kweli mtu huyu amefanya kosa lolote.”+

6 Kwa hiyo, baada ya kukaa kati yao siku zisizozidi nane au kumi, akashuka kwenda Kaisaria, na siku iliyofuata akaketi kwenye kiti cha hukumu na kuamuru Paulo aletwe. 7 Alipoingia, Wayahudi waliokuwa wameshuka kutoka Yerusalemu wakasimama kumzunguka, wakitoa mashtaka mengi mazito ambayo hawakuweza kuyathibitisha.+

8 Lakini Paulo akajitetea hivi: “Sijatenda dhambi yoyote dhidi ya Sheria ya Wayahudi wala dhidi ya hekalu wala dhidi ya Kaisari.”+ 9 Festo akitamani kukubaliwa na Wayahudi,+ akamjibu Paulo: “Je, ungependa kupanda kwenda Yerusalemu ukahukumiwe huko mbele yangu kuhusu mambo haya?” 10 Lakini Paulo akasema: “Mimi nimesimama mbele ya kiti cha hukumu cha Kaisari, ambapo ninapaswa kuhukumiwa. Sijawakosea Wayahudi, nawe pia umegundua jambo hilo. 11 Ikiwa, kwa kweli mimi ni mkosaji na nimefanya jambo lolote linalostahili kifo,+ niko tayari kufa; lakini kama mashtaka ya watu hawa hayana msingi, hakuna mtu aliye na haki ya kunikabidhi kwao ili tu apate kibali chao. Ninakata rufaa kwa Kaisari!”+ 12 Ndipo Festo, baada ya kuzungumza na baraza la washauri, akajibu: “Umekata rufaa kwa Kaisari; nawe utaenda kwa Kaisari.”

13 Baada ya siku kadhaa, Agripa mfalme na Bernike wakafika Kaisaria kwa ajili ya ziara ya kumsalimia Festo. 14 Kwa kuwa wangekaa huko siku kadhaa, Festo akawasilisha kesi ya Paulo mbele ya mfalme, akisema:

“Kuna mwanamume ambaye Feliksi alimwacha akiwa mfungwa, 15 nami nilipokuwa Yerusalemu wakuu wa makuhani na wazee wa Wayahudi walileta habari kumhusu,+ wakiomba ahukumiwe hatia. 16 Lakini nikawajibu kwamba si utaratibu wa Kiroma kumkabidhi mtu yeyote ili tu kupata kibali kabla ya mshtakiwa kukutana uso kwa uso na wale waliomshtaki na kupata nafasi ya kujitetea kuhusu mashtaka.+ 17 Basi walipofika hapa, sikukawia, bali kesho yake niliketi kwenye kiti cha hukumu na kuamuru mwanamume huyo aletwe. 18 Wale waliomshtaki waliposimama, hawakumshtaki kwa mambo maovu niliyotazamia.+ 19 Ila tu walikuwa wakibishana naye kuhusu ibada yao ya mungu*+ na kuhusu mtu fulani anayeitwa Yesu ambaye alikufa, lakini ambaye Paulo alikuwa akisisitiza kwamba yuko hai.+ 20 Sikujua jinsi ya kutatua mabishano haya, basi nikamuuliza kama angependa kwenda Yerusalemu ili akahukumiwe huko kuhusu mambo haya.+ 21 Lakini Paulo alipokata rufaa ili abaki kizuizini akisubiri uamuzi wa Augusto Mkuu,*+ nikaamuru azuiliwe mpaka nitakapomtuma kwa Kaisari.”

22 Ndipo Agripa akamwambia Festo: “Mimi mwenyewe ningependa kumsikia mtu huyo.”+ Akasema: “Kesho utamsikia.” 23 Basi kesho yake, Agripa na Bernike wakaja kwa fahari nyingi na kuingia katika ukumbi wa baraza pamoja na viongozi wa jeshi na vilevile wanaume mashuhuri wa jiji; naye Festo alipotoa amri, Paulo akaletwa. 24 Festo akasema: “Mfalme Agripa na nyote mlio hapa pamoja nasi, mnamwona mtu huyu ambaye Wayahudi wote wameniomba huko Yerusalemu na huku pia, wakipaza sauti kwamba hapaswi kuendelea kuishi.+ 25 Lakini nikaona kwamba hakuwa amefanya jambo lolote linalostahili kifo.+ Basi mtu huyu alipokata rufaa kwa Augusto Mkuu, niliamua kumpeleka. 26 Lakini sina jambo hususa la kumwandikia Bwana wangu kumhusu. Basi nimemleta mbele yenu nyote, na hasa mbele yako wewe, Mfalme Agripa, ili baada ya kumchunguza kihukumu, nipate jambo la kuandika. 27 Kwa maana ninaona haifai kumpeleka mfungwa bila kuonyesha mashtaka yanayomkabili.”

26 Agripa+ akamwambia Paulo: “Unaruhusiwa kujitetea.” Ndipo Paulo akanyoosha mkono wake na kuanza kujitetea:

2 “Kuhusu mambo yote ninayoshtakiwa na Wayahudi,+ Mfalme Agripa, ninafurahi kwamba ninajitetea mbele yako leo, 3 hasa kwa sababu wewe una ujuzi mwingi kuhusu desturi zote na vilevile mabishano kati ya Wayahudi. Kwa hiyo, ninakuomba unisikilize kwa subira.

4 “Kwa kweli, maisha niliyoishi tangu ujana miongoni mwa watu wangu* na huko Yerusalemu yanajulikana vizuri na Wayahudi wote+ 5 ambao mwanzoni walinifahamu, nao wakipenda wanaweza kutoa ushahidi kwamba niliishi nikiwa Farisayo+ kulingana na madhehebu yetu yenye msimamo mkali zaidi katika ibada yetu.+ 6 Lakini sasa, kwa sababu ya tumaini la ahadi iliyotolewa na Mungu kwa mababu zetu,+ nimeitwa kwenye hukumu; 7 makabila yetu 12 yanatumaini kuona ahadi hiyo ikitimizwa kwa kumtolea Mungu utumishi mtakatifu kwa bidii usiku na mchana. Wayahudi wananishtaki kwa sababu ya tumaini hili,+ ewe Mfalme.

8 “Kwa nini mnafikiri* kwamba ni jambo lisilowezekana kwa Mungu kuwafufua wafu? 9 Mimi niliamini kwamba ninapaswa kufanya matendo mengi ili kulipinga jina la Yesu Mnazareti. 10 Hivyo ndivyo nilivyofanya huko Yerusalemu, niliwafunga gerezani watakatifu wengi,+ kwa maana nilikuwa nimepewa mamlaka na wakuu wa makuhani;+ na walipopaswa kuuawa, nilipiga kura yangu dhidi yao. 11 Niliwaadhibu mara nyingi katika masinagogi yote, nikijaribu kuwalazimisha wakane imani yao; na kwa sababu nilikuwa nimewakasirikia sana, nilifikia hatua ya kuwatesa hata katika majiji yaliyo mbali.

12 “Nilipokuwa nikifanya hivyo nikiwa safarini kwenda Damasko pia nikiwa na mamlaka na maagizo kutoka kwa wakuu wa makuhani, 13 katikati ya mchana niliona barabarani, ewe Mfalme, nuru kutoka mbinguni inayozidi mwangaza wa jua ikimulika kunizunguka mimi na wale waliokuwa wakisafiri pamoja nami.+ 14 Sisi sote tulipoanguka chini, nikasikia sauti ikiniambia katika lugha ya Kiebrania: ‘Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa? Kuendelea kuipiga teke michokoo* kunafanya iwe vigumu kwako.’⁠ 15 Lakini nikauliza: ‘Wewe ni nani Bwana?’ Naye Bwana akajibu: ‘Mimi ni Yesu, ambaye unamtesa. 16 Hata hivyo, inuka usimame kwa miguu yako. Kwa sababu nimekutokea ili nikuchague uwe mtumishi na shahidi wa mambo ambayo umeona na pia mambo nitakayokuonyesha kunihusu.+ 17 Nami nitakuokoa kutoka kwa watu hawa na kutoka kwa mataifa ambayo ninakutuma kwao+ 18 ili kuwafungua macho,+ kuwageuza watoke gizani+ waingie kwenye nuru+ na watoke kwenye mamlaka ya Shetani+ wamgeukie Mungu, ili wasamehewe dhambi zao+ na kupata urithi miongoni mwa wale waliotakaswa kwa kuniamini mimi.’

19 “Kwa hiyo, Mfalme Agripa, mimi sikukosa kutii maono hayo kutoka mbinguni, 20 lakini kwanza kwa wale walio huko Damasko+ kisha kwa wale walio Yerusalemu,+ na katika nchi yote ya Yudea, na pia kwa mataifa, nilikuwa nikipeleka ujumbe kwamba wanapaswa kutubu na kumgeukia Mungu kwa kufanya matendo yanayoonyesha toba.+ 21 Hiyo ndiyo sababu Wayahudi walinikamata hekaluni na kujaribu kuniua.+ 22 Hata hivyo, kwa sababu nimepata msaada kutoka kwa Mungu, mpaka leo hii ninaendelea kutoa ushahidi kwa wadogo na wakubwa pia, bila kusema lolote zaidi ya yale ambayo Manabii na pia Musa walisema yatatukia+— 23 kwamba Kristo atateseka+ na akiwa wa kwanza kufufuliwa kutoka kwa wafu,+ atawatangazia nuru watu hawa na pia mataifa.”+

24 Paulo alipokuwa akijitetea kwa kusema mambo hayo, Festo akasema kwa sauti kubwa: “Unarukwa na akili, Paulo! Kusoma kwingi kunafanya urukwe na akili!” 25 Lakini Paulo akasema: “Mimi sirukwi na akili, ewe Mtukufu Festo, bali ninasema maneno ya kweli na ya akili timamu. 26 Kwa kweli, mfalme ninayezungumza naye kwa uhuru anajua vizuri mambo haya; nina hakika kwamba hakuna hata moja kati ya mambo haya ambalo hajui, kwa maana hakuna jambo lolote lililofanywa kisiri.+ 27 Je, wewe, Mfalme Agripa, unawaamini Manabii? Ninajua unawaamini.” 28 Lakini Agripa akamwambia Paulo: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.” 29 Ndipo Paulo akasema: “Ninamwomba Mungu kwamba iwe ni kwa muda mfupi au muda mrefu, si wewe tu bali pia wote wanaonisikia leo wawe kama mimi nilivyo, ila tu bila vifungo hivi vya gereza.”

30 Ndipo mfalme akasimama, vilevile gavana na Bernike na watu walioketi pamoja nao. 31 Lakini walipokuwa wakiondoka wakaanza kuambiana: “Mtu huyu hafanyi lolote linalostahili kifo au vifungo vya gereza.”+ 32 Kisha Agripa akamwambia Festo: “Mtu huyu angefunguliwa kama hangekuwa amekata rufaa kwa Kaisari.”+

27 Basi kwa kuwa iliamuliwa tusafiri baharini kwenda Italia,+ wakamkabidhi Paulo na wafungwa wengine kwa ofisa wa jeshi anayeitwa Yulio, wa kikosi cha Augusto. 2 Tukapanda meli kutoka Adramitiamu iliyokuwa karibu kusafiri kwenda kwenye bandari zilizo kando ya pwani ya mkoa wa Asia, tukaanza safari; naye Aristarko+ Mmakedonia wa Thesalonike, alikuwa pamoja nasi. 3 Siku iliyofuata tukafika Sidoni, na Yulio akamtendea Paulo kwa fadhili* na kumruhusu aende kwa rafiki zake akatunzwe nao.

4 Tulipotoka huko, tukasafiri karibu na Kipro ili kujikinga na pepo zilizokuwa zikivuma kinyume nasi. 5 Kisha tukapita kwenye bahari kuu kandokando ya Kilikia na Pamfilia na kutia nanga kwenye bandari ya Mira huko Likia. 6 Huko ofisa wa jeshi akapata meli kutoka Aleksandria iliyokuwa ikielekea Italia, naye akatuagiza tupande meli hiyo. 7 Kisha baada ya kusafiri polepole kwa siku kadhaa, tukafika kwa shida huko Kinido. Kwa sababu upepo ulituzuia kusonga mbele, tukasafiri chini ya Krete karibu na Salmone. 8 Tukasafiri kwa shida kandokando ya pwani, tukafika mahali panapoitwa Bandari Nzuri, karibu na jiji la Lasea.

9 Muda mrefu ulikuwa umepita na kufikia sasa ilikuwa hatari kusafiri baharini, kwa sababu hata kipindi cha kufunga kwa Siku ya Kufunika Dhambi+ tayari kilikuwa kimepita, basi Paulo akatoa pendekezo, 10 akawaambia: “Ninaona kwamba safari hii itakuwa na madhara na hasara kubwa si kwa shehena na meli tu bali pia kwa uhai wetu.”* 11 Hata hivyo, ofisa wa jeshi akamsikiliza nahodha na mwenye meli badala ya kusikiliza alichokuwa akisema Paulo. 12 Kwa kuwa bandari hiyo haikufaa wakati wa majira ya baridi kali, wengi wakapendekeza kuendelea na safari, ili kuona kama wangefaulu kukaa wakati wa majira ya baridi kali huko Feniki, ambayo ni bandari ya Krete inayofunguka kuelekea kaskazini mashariki na kuelekea kusini mashariki.

13 Upepo wa kusini ulipovuma kwa utulivu, walifikiri kwamba wametimiza kusudi lao, wakang’oa nanga na kuanza kusafiri kandokando ya Krete karibu na ufuo. 14 Hata hivyo, baada ya muda mfupi, upepo mkali unaoitwa Euroakilo* ukavuma kwa kasi juu yake. 15 Kwa kuwa meli ilipigwa na upepo wenye nguvu na ikashindwa kuukabili, tukaiachilia nao upepo ukatusukuma. 16 Kisha tukapita chini ya kisiwa kidogo kinachoitwa Kauda, na bado ilikuwa vigumu kuiokoa mashua ndogo* iliyokuwa kwenye tezi ya meli. 17 Lakini baada ya kuiingiza ndani, wakaifunga ile mashua kwenye meli, na kwa kuwa waliogopa kukwama kwenye mchanga wa Sirti,* wakashusha vifaa vya kuendeshea na hivyo wakasukumwa na upepo. 18 Kwa sababu tulikuwa tukirushwarushwa kwa nguvu na dhoruba, siku iliyofuata wakaanza kupunguza uzito wa meli. 19 Siku ya tatu, wakatupa ayari za meli hiyo kwa mikono yao wenyewe.

20 Tulipokosa kuona jua wala nyota kwa siku nyingi na kupigwa na dhoruba kali,* mwishowe tulianza kupoteza tumaini la kuokoka. 21 Baada ya watu kukaa kwa muda mrefu bila kula, Paulo alisimama katikati yao na kusema: “Ikiwa mngefuata ushauri wangu hamngesafiri baharini kutoka Krete na hivyo hamngepatwa na madhara na hasara hii.+ 22 Hata hivyo, sasa ninawahimiza mjipe moyo, kwa maana hakuna hata mmoja wenu atakayepotea,* meli tu ndiyo itakayopotea. 23 Usiku huu malaika+ wa Mungu ambaye mimi ni mali yake na ambaye ninamtolea utumishi mtakatifu, alisimama kando yangu 24 akasema: ‘Usiogope, Paulo. Utasimama mbele ya Kaisari,+ na tazama! Mungu amekupa wale wote wanaosafiri pamoja nawe.’ 25 Basi jipeni moyo, kwa maana ninamwamini Mungu kwamba itakuwa kama nilivyoambiwa. 26 Hata hivyo, ni lazima tutupwe kwenye ufuo wa kisiwa fulani.”+

27 Sasa usiku wa 14 ulipofika nasi tukawa tukirushwa huku na huku katika Bahari ya Adria, katikati ya usiku mabaharia walianza kuhisi kwamba walikuwa wakikaribia nchi kavu. 28 Wakapima kina kwa bildi na kupata pima 20,* basi wakasonga mbele kidogo wakapima tena na kupata pima 15.* 29 Wakiogopa kwamba tungekwama kwenye miamba, wakashusha nanga nne kutoka kwenye tezi na kuanza kutamani kupambazuke. 30 Lakini mabaharia walipojaribu kutoroka kutoka kwenye meli na kushusha mashua ndogo ndani ya bahari wakisingizia kwamba walikusudia kuzishusha nanga kutoka kwenye omo, 31 Paulo akamwambia ofisa wa jeshi na wanajeshi: “Watu hawa wasipobaki katika meli, ninyi hamwezi kuokoka.”+ 32 Ndipo wanajeshi wakakata kamba za ile mashua ndogo na kuiacha ianguke.

33 Sasa kulipokaribia kupambazuka, Paulo akawahimiza wote wale chakula, akisema: “Kwa siku 14 mmekuwa mkisubiri kwa wasiwasi, bila kula chochote. 34 Basi ninawatia moyo mle chakula; kwa ajili ya usalama wenu, kwa maana hakuna hata unywele mmoja wa vichwa vyenu utakaopotea.” 35 Baada ya kusema hivyo, akachukua mkate, akamshukuru Mungu mbele yao wote, akaumega, na kuanza kula. 36 Kwa hiyo wote wakajipa moyo, nao pia wakaanza kula. 37 Kwa ujumla, sote tulikuwa watu* 276 katika meli. 38 Walipokula chakula wakashiba, wakapunguza uzito wa meli kwa kutupa ngano baharini.+

39 Kulipopambazuka, hawakuitambua nchi hiyo,+ lakini waliona ghuba yenye ufuo, nao waliazimia kuipeleka meli ufuoni kama wangeweza. 40 Basi wakazikata nanga na kuziacha zianguke baharini, wakati huohuo wakifungua kamba za makasia ya usukani; na baada ya kutweka tanga la mbele kwenye upepo, wakaelekea ufuoni. 41 Wakagonga rundo kubwa la mchanga lililorundikwa na bahari pande zote, wakaendesha meli juu ya mchanga nayo omo ikakwama na kukaa bila kutikisika, lakini mawimbi yakaanza kuvunja tezi vipandevipande kwa nguvu.+ 42 Ndipo wanajeshi wakaamua kuwaua wafungwa ili yeyote asiogelee na kutoroka. 43 Lakini ofisa wa jeshi alikuwa ameazimia kumfikisha Paulo salama naye akawazuia ili wasitekeleze mpango wao. Akawaamuru wale ambao wangeweza kuogelea wajitupe baharini na watangulie kuogelea mpaka nchi kavu, 44 na wale wengine wangefuata, wengine wakiwa juu ya mbao na wengine juu ya vipande vya meli. Basi wote wakafika salama kwenye nchi kavu.+

28 Tulipofika salama ufuoni, tukajua kwamba kisiwa hicho kiliitwa Malta.+ 2 Na watu hao waliozungumza lugha ya kigeni* walitutendea kwa fadhili zinazopita za kawaida.* Wakawasha moto na kutukaribisha sote kwa fadhili kwa sababu mvua ilikuwa ikinyesha na kulikuwa na baridi. 3 Lakini Paulo alipokusanya tita la kuni na kuliweka juu ya moto, nyoka* akatoka kwa sababu ya joto na kujifunga kwenye mkono wake. 4 Watu hao waliozungumza lugha ya kigeni walipomwona nyoka huyo mwenye sumu akining’inia kwenye mkono wake, wakaanza kuambiana: “Hakika mtu huyu ni muuaji, na ingawa alifika salama kutoka baharini, Haki* haikumruhusu aendelee kuishi.” 5 Hata hivyo, akamkung’uta yule nyoka na kumtupa ndani ya moto, naye hakupatwa na madhara. 6 Lakini walitarajia kwamba atavimba au aanguke na kufa ghafla. Baada ya kusubiri kwa muda mrefu na kuona hajapatwa na jambo lolote baya, wakabadili maoni yao na kuanza kusema yeye ni mungu.

7 Sasa karibu na mahali hapo kulikuwa na mashamba ya mkuu wa kisiwa hicho, aliyeitwa Publio, ambaye alitukaribisha na kutuonyesha ukarimu kwa siku tatu. 8 Ikawa kwamba baba ya Publio alikuwa amelala kitandani akiugua homa na ugonjwa wa kuhara damu. Paulo akaingia alimokuwa na kusali, akaweka mikono juu yake, akamponya.+ 9 Baada ya tukio hilo, wote waliokuwa wagonjwa katika kisiwa hicho wakaanza pia kuja kwake na kuponywa.+ 10 Pia wakatupatia zawadi nyingi, na tulipokuwa tukianza safari, wakapakia melini vitu vyote tulivyohitaji.

11 Miezi mitatu baadaye tukasafiri kwa meli ambayo upande wa mbele ilikuwa na sanamu ya “Wana wa Zeu.” Meli hiyo ilitoka Aleksandria na ilikuwa imekaa kwenye kisiwa hicho wakati wa majira ya baridi kali. 12 Tukatia nanga katika bandari ya Sirakusa tukakaa huko siku tatu; 13 kutoka hapo tukasafiri mpaka Regiamu. Siku moja baadaye, upepo wa kusini ukaanza kuvuma nasi tukaingia Puteoli siku ya pili. 14 Tukawakuta akina ndugu huko, wakatusihi tukae pamoja nao kwa siku saba, kisha tukaelekea Roma. 15 Kutoka huko, akina ndugu waliposikia habari zetu, wakaja mpaka Soko la Apio na Mikahawa Mitatu ili kutupokea. Paulo alipowaona, akamshukuru Mungu na kujipa moyo.+ 16 Mwishowe, tulipoingia Roma, Paulo aliruhusiwa kukaa peke yake akiwa na mwanajeshi aliyemlinda.

17 Hata hivyo, baada ya siku tatu akawaita wanaume mashuhuri wa Wayahudi. Walipokuwa wamekusanyika, akawaambia: “Wanaume, akina ndugu, ingawa sikuwa nimefanya jambo lolote kinyume cha watu au desturi za mababu zetu,+ nilikabidhiwa nikiwa mfungwa kutoka Yerusalemu na kutiwa mikononi mwa Waroma.+ 18 Na baada ya kufanya uchunguzi,+ walitaka kuniacha huru, kwa maana hawakuwa na sababu yoyote ya kuniua.+ 19 Lakini Wayahudi walipopinga, nililazimika kukata rufaa kwa Kaisari,+ lakini si kwa sababu nilikuwa na shtaka lolote dhidi ya taifa langu. 20 Basi kwa sababu hii niliomba kuwaona na kuzungumza nanyi, kwa maana nimefungwa mnyororo huu kwa sababu ya tumaini la Israeli.”+ 21 Wakamwambia: “Hatujapokea barua zozote kukuhusu kutoka Yudea, wala hakuna ndugu yeyote aliyekuja kutoka huko ambaye ametujulisha au kusema jambo lolote baya juu yako. 22 Lakini tunaona inafaa kusikia kutoka kwako maoni yako, kwa maana kwa kweli kuhusu madhehebu haya,+ tunajua yanasemwa vibaya kila mahali.”+

23 Basi wakapanga siku ya kukutana pamoja naye, nao wakaja wakiwa wengi hata zaidi mahali alipoishi. Na kuanzia asubuhi mpaka jioni, akawafafanulia jambo hilo na kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu, ili kuwashawishi kumhusu Yesu+ kwa kutumia Sheria ya Musa+ na pia Manabii.+ 24 Baadhi yao wakaanza kuamini mambo aliyosema; lakini wengine hawakuamini. 25 Basi kwa sababu hawakukubaliana miongoni mwao, wakaanza kuondoka, naye Paulo akasema jambo hili moja:

“Kwa kufaa roho takatifu ilisema kupitia Isaya nabii kwa mababu zenu, 26 ikisema, ‘Nenda kwa watu hawa uwaambie: “Kwa kweli mtasikia lakini hamtaelewa kamwe, na kwa kweli mtatazama, lakini hamtaona kamwe.+ 27 Kwa maana mioyo ya watu hawa imekuwa migumu, nao wamesikia kwa masikio yao bila kuitikia, nao wamefunga macho yao, ili wasione kamwe kwa macho yao na kusikia kwa masikio yao na kuelewa kwa mioyo yao, nao wageuke nami niwaponye.”’+ 28 Basi jueni kwamba wokovu huu kutoka kwa Mungu umepelekwa kwa mataifa;+ nao kwa hakika watausikiliza.”+ 29* ——

30 Kwa hiyo akakaa huko kwa miaka miwili kamili katika nyumba yake ya kukodi,+ naye alikuwa akiwakaribisha kwa fadhili wale wote waliomtembelea, 31 akiwahubiria Ufalme wa Mungu na kuwafundisha kumhusu Bwana Yesu Kristo kwa uhuru mwingi wa kusema,*+ bila kizuizi.

Au “miisho.”

Au “umati wa.”

Au “akapasuka katikati.”

Au, “alipoingia na kutoka.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “akajumlishwa,” yaani, akaonwa sawa na wale wengine 11.

Au “ndimi.”

Au “lugha yake ya kuzaliwa.”

Au “divai mpya.”

Yaani, karibu saa 3 asubuhi.

Au “miujiza.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “miujiza.”

Au “shauri lililoamuliwa.”

Au labda, “kamba za.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “mbele ya macho yangu.”

Tnn., “mwili wangu utaishi.”

Au “hutaiacha nafsi yangu.”

Au “Hadesi.” Angalia Kamusi.

Au “hutaruhusu mwili wake uoze.”

Au “mbele za uso wako.”

Tnn., “mmoja kati ya wazao wa kiuno chake.”

Au “Hadesi.” Angalia Kamusi.

Au “haukuoza.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “nafsi 3,000 zikaongezeka.”

Au “kushiriki vitu na wengine.”

Au “kila nafsi ikawa.”

Au “miujiza mingi.”

Angalia Nyongeza A5.

Yaani, karibu saa 9 alasiri.

Angalia Kamusi.

Tnn., “kutoka kwa uso wa Yehova.” Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “nafsi yoyote.”

Tnn., “mbegu yako.”

Au “kufufuliwa kutoka kwa wafu katika kisa cha Yesu.”

Tnn., “kichwa cha pembeni.”

Yaani, hawakuwa na elimu ya shule za kirabi; haimaanishi hawakujua kusoma na kuandika.

Au “ishara hiyo.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “Kristo wake.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “miujiza.”

Au “waliposali kwa bidii.”

Angalia Kamusi.

Angalia Nyongeza A5.

Au “miujiza.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “wakahisi wamechomwa.”

Tnn., “Haipendezi.”

Au “miujiza.”

Tnn., “mbegu yake.”

Tnn., “mbegu.”

Au “kuwatendea vibaya.”

Au labda, “akafanya vivyo hivyo na.”

Au “wazee wetu wa ukoo.”

Au “nafaka.”

Au “nafsi.”

Au “Akalelewa.”

Au “alipotupwa.”

Au “akaamua.”

Au “awakague.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “miujiza.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “wakachomwa.”

Angalia Nyongeza A5.

Au labda, “mojawapo ya majiji ya Samaria.”

Angalia Nyongeza A5.

Tnn., “nyongo ya uchungu.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “ofisa wa makao ya mfalme.”

Au “unaelewa.”

Angalia Nyongeza A3.

Angalia Nyongeza A5.

Tnn., “awafunge; awatie vifungoni.”

Tnn., “kuwaongoza wakiwa wamefungwa.”

Tnn., “akiingia na kutoka.”

Angalia Nyongeza A5.

Jina la Kigiriki Dorkasi na jina la Kiaramu Tabitha, yote yanamaanisha “Swala.”

Au “mavazi ya nje.”

Ofisa aliyesimamia wanajeshi 100.

Kikosi cha jeshi la Roma chenye wanajeshi 600.

Yaani, karibu saa 9 alasiri.

Yaani, karibu saa 6 mchana.

Tnn., “chombo cha aina fulani.”

Au “kumwinamia.”

Yaani, karibu saa 9 alasiri.

Angalia Nyongeza A5.

Au “kumfanya aonekane.”

Au “waaminifu.”

Tnn., “ndimi.”

Au “kushindana naye.”

Tnn., “chombo cha aina fulani.”

Au “kumpinga.”

Tnn., “wakanyamaza.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “huduma ya msaada.”

Au “kumtoa ili ahukumiwe.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “Jifunge.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “alitaka kupigana na.”

Tnn., “chumba cha kulala cha mfalme.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “wakimhudumia hadharani.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “akiwasaidia”

Gavana Mroma aliyesimamia mkoa. Angalia Kamusi.

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Tnn., “mbegu ya.”

Au “kwenye kaburi la ukumbusho.”

Au “wenye kutegemeka.”

Au “aoze.”

Au “alifanya mapenzi ya Mungu.”

Au “na mwili wake ukaoza.”

Au “hakuoza.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “nafsi za watu.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “miujiza.”

Au “wakazitia nguvu nafsi za wanafunzi.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “bishano.”

Au “kubishana sana.”

Au “miujiza.”

Au “ kibanda cha; nyumba ya.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “maoni yangu.”

Neno la Kigiriki porneiʹa. Angalia Kamusi.

Au “wanyama waliouawa bila kutolewa damu.”

Au “kuzivuruga nafsi zenu.”

Au “nafsi zao.”

Au “wanyama waliouawa bila kutolewa damu.”

Neno la Kigiriki porneiʹa. Angalia Kamusi.

Au “Kwaherini.”

Angalia Nyongeza A3.

Angalia Nyongeza A5.

Au labda, “Kwa vyovyote vile turudi.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “wakapitia.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “kupiga ramli.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “bila uamuzi wa mahakama.”

Au “wameleta vurugu katika.”

Au “waliotembelea.”

Au “mnapenda sana dini.”

Au “uzao.”

Au “uzao.”

Au “Alikuwa akijadiliana nao.”

Yaani, sinagogi.

Gavana Mroma aliyetawala mkoa. Angalia Kamusi.

Angalia Nyongeza A5.

Inaonekana alienda Yerusalemu.

Au “amefundishwa kwa mdomo.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “wakawa wakaidi.”

Angalia Nyongeza A5.

Liwali alikuwa gavana Mroma aliyetawala mkoa. Angalia Kamusi.

Au “nafsi yake imo ndani yake.”

Tnn., “akaumega mkate.”

Au “unyenyekevu wa akili.”

Au “kwa faida yenu.”

Au “nimechochewa na.”

Au “nafsi yangu.”

Au “ukiwa na thamani yoyote kwangu.”

Au “kusudi lote la.”

Tnn., “wakamwangukia Paulo shingoni.”

Au “wororo.”

Tnn., “walikuwa mabikira.”

Au “kuudhoofisha moyo wangu.”

Tnn., “tukakaa kimya.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “ vitu vilivyouawa bila kutolewa damu.”

Neno la Kigiriki porneiʹa. Angalia Kamusi.

Au “raia Mroma.”

Au “bila uamuzi wa mahakama.”

Au “huyatangaza hadharani.”

Au “kiapo.”

Au “kiapo.”

Au “mwanasheria.”

Tnn., “tauni.”

Angalia Nyongeza A3.

Au “dhamiri isiyo na lawama.”

Au “kujidhibiti; kujiweza.”

Tnn., “kibali dhidi yake.”

Au “dini yao.”

Jina la cheo la maliki Mroma.

Au “taifa langu.”

Tnn., “mnahukumu.”

Mchokoo ni fimbo yenye ncha iliyochongoka inayotumiwa kumwelekeza mnyama.

Au “fadhili za kibinadamu.”

Au “nafsi zetu.”

Yaani, upepo wa kaskazini mashariki.

Mashua ndogo inayotumiwa kuokoa uhai.

Angalia Kamusi.

Tnn., “isiyo ndogo.”

Au “nafsi itakayopotea.”

Karibu mita 36 (futi 120). Angalia Nyongeza B14.

Karibu mita 27 (futi 90). Angalia Nyongeza B14.

Au “nafsi.”

Au “wenyeji wa nchi hiyo.”

Au “fadhili za kibinadamu.”

Au “nyoka-kipiri.”

Neno la Kigiriki Diʹke, ambalo huenda linarejelea mungu wa kike wa kulipiza kisasi au wazo la haki ya kudhaniwa.

Angalia Nyongeza A3.

Au “kwa ujasiri wote.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki