YOSHUA
1 Baada ya kifo cha Musa mtumishi wa Yehova, Yehova akamwambia Yoshua*+ mwana wa Nuni, mhudumu+ wa Musa: 2 “Musa mtumishi wangu amekufa.+ Sasa jitayarishe, vuka Mto Yordani pamoja na watu hawa wote, mwingie katika nchi ambayo ninawapa Waisraeli.+ 3 Nitawapa kila mahali mtakapokanyaga, kama nilivyomwahidi Musa.+ 4 Eneo lenu litaanzia nyikani mpaka kwenye Mlima Lebanoni hadi ule mto mkubwa, Efrati, yaani, nchi yote ya Wahiti,+ mpaka kwenye Bahari Kuu,* upande wa magharibi.*+ 5 Hakuna yeyote atakayekushinda sikuzote za maisha yako.+ Nitakuwa pamoja nawe kama nilivyokuwa pamoja na Musa.+ Sitakutupa wala kukuacha.+ 6 Uwe jasiri na imara,+ kwa sababu ni wewe utakayewaongoza watu hawa kuirithi nchi niliyowaapia mababu zao kwamba nitawapa.+
7 “Ila tu uwe jasiri na imara kabisa, na ufuate kwa uangalifu Sheria yote kama Musa mtumishi wangu alivyokuamuru. Usiende kushoto wala kulia,+ ili utende kwa hekima mahali popote utakapoenda.+ 8 Kitabu hiki cha Sheria kisiondoke kinywani mwako,+ ni lazima ukisome kwa sauti ya chini* mchana na usiku ili ufuate kwa uangalifu mambo yote yaliyoandikwa humo;+ ndipo utakapofanikisha njia yako na kutenda kwa hekima.+ 9 Je, si mimi niliyekuamuru uwe jasiri na imara? Basi uwe jasiri na imara. Usitetemeke wala kuogopa, kwa maana mimi Yehova Mungu wako nipo pamoja nawe mahali popote utakapoenda.”+
10 Ndipo Yoshua akawaamuru viongozi wa watu akisema, 11 “Piteni katika kambi yote na kuwaamuru watu hivi: ‘Tayarisheni vyakula, kwa sababu baada ya siku tatu mtavuka Mto Yordani ili kuingia na kuimiliki nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa.’”+
12 Kisha Yoshua akawaambia hivi watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase: 13 “Kumbukeni amri ambayo Musa mtumishi wa Yehova aliwapa aliposema,+ ‘Yehova Mungu wenu anawapumzisha, naye amewapa nchi hii. 14 Wake zenu, watoto wenu, na wanyama wenu wa kufugwa watakaa katika nchi ambayo Musa amewapa upande huu* wa Yordani,+ lakini ninyi nyote mashujaa hodari+ mnapaswa kuvuka na kuwatangulia ndugu zenu mkiwa mmejipanga kivita.+ Mnapaswa kuwasaidia 15 mpaka Yehova atakapowapa ndugu zenu mahali pa kupumzika, kama alivyowapa ninyi, nao pia wamiliki nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa. Kisha rudini na kuimiliki nchi yenu ambayo Musa mtumishi wa Yehova aliwapa upande wa mashariki wa Yordani.’”+
16 Wakamwambia Yoshua: “Tutafanya yote ambayo umetuamuru, na tutaenda mahali popote unapotaka twende.+ 17 Kama tulivyomtii Musa katika mambo yote, ndivyo tutakavyokutii. Yehova Mungu wako na awe pamoja nawe kama alivyokuwa pamoja na Musa.+ 18 Mtu yeyote atakayeasi agizo lako na asiyetii amri yoyote utakayotoa atauawa.+ Lakini uwe jasiri na imara.”+
2 Kisha Yoshua mwana wa Nuni akawatuma kwa siri wanaume wawili wapelelezi kutoka Shitimu,+ akawaambia: “Nendeni mkaipeleleze nchi, hasa jiji la Yeriko.” Basi wakaenda na kufika nyumbani kwa mwanamke mmoja kahaba aliyeitwa Rahabu,+ wakakaa humo. 2 Mfalme wa Yeriko akaambiwa: “Wanaume Waisraeli wameingia humu leo usiku ili kuipeleleza nchi.” 3 Ndipo mfalme wa Yeriko akawatuma wajumbe kwa Rahabu, akisema: “Watoe nje wanaume waliokuja nyumbani mwako, kwa sababu wamekuja kuipeleleza nchi nzima.”
4 Lakini mwanamke huyo alikuwa amewaficha wanaume hao wawili. Basi akasema: “Ni kweli, wanaume hao walikuja kwangu, lakini sikujua walikotoka. 5 Giza lilipoingia, waliondoka kabla ya lango la jiji kufungwa. Sijui walikokwenda, mkiwafuatia haraka, mtawafikia.” 6 (Lakini alikuwa amewaficha juu ya paa katikati ya majani ya kitani yaliyopangwa paani.) 7 Basi watu hao wakawafuatia kwenye vivuko vya Yordani,+ na mara tu walipotoka, lango la jiji likafungwa.
8 Kabla wapelelezi hao hawajalala, Rahabu akaenda kuwaona kwenye paa. 9 Akawaambia: “Najua kwamba Yehova atawapa nchi hii+ na tumeshikwa na hofu kwa sababu yenu.+ Wakaaji wote wa nchi wamevunjika moyo kwa sababu yenu,+ 10 kwa maana tumesikia jinsi Yehova alivyoyakausha maji ya Bahari Nyekundu* mbele yenu mlipotoka Misri+ na mambo mliyowatendea wale wafalme wawili wa Waamori, yaani, Sihoni+ na Ogu,+ waliokuwa ng’ambo ya* Yordani, mliowaangamiza kabisa. 11 Tuliposikia hayo, tulikufa moyo,* na hakuna yeyote aliye na ujasiri kwa sababu yenu, kwa kuwa Yehova Mungu wenu ni Mungu juu mbinguni na chini duniani.+ 12 Sasa, tafadhalini, niapieni kwa Yehova kwamba, kwa kuwa nimewatendea kwa upendo mshikamanifu, ninyi pia mtaitendea familia ya baba yangu kwa upendo mshikamanifu; nipeni ishara inayoaminika* kwamba mtatimiza ahadi yenu. 13 Nanyi hamtawaangamiza baba yangu na mama yangu, ndugu zangu na dada zangu, na watu wetu wote, mtatuokoa tusife.”*+
14 Ndipo wanaume hao wakamwambia: “Tutakufa badala yenu!* Ikiwa hamtatoa habari kuhusu mambo yaliyotuleta, tutawatendea kwa upendo mshikamanifu na kwa uaminifu Yehova atakapotupatia nchi hii.” 15 Basi akawashusha kwa kamba kupitia dirishani, kwa kuwa nyumba yake ilikuwa imejengwa kwenye ukuta wa jiji.+ 16 Naye akawaambia: “Nendeni milimani mkajifiche huko kwa siku tatu ili wale wanaowafuatia wasiwapate. Kisha wakirudi mnaweza kwenda zenu.”
17 Wanaume hao wakasema: “Hatutakuwa na hatia kuhusiana na kiapo ulichotuapisha+ 18 isipokuwa, tutakapokuja katika nchi hii, utakuwa umefunga kamba hii nyekundu katika dirisha ambamo utatuteremshia. Wakusanye baba yako, mama yako, ndugu zako, na familia yote ya baba yako ndani ya nyumba hii.+ 19 Ikiwa mtu yeyote atatoka nje ya nyumba yako, damu yake itakuwa juu ya kichwa chake mwenyewe, nasi hatutakuwa na hatia. Lakini mtu yeyote aliye ndani ya nyumba yako pamoja nawe akifa, damu yake itakuwa juu ya vichwa vyetu. 20 Lakini ukitoa habari kuhusu mambo yaliyotuleta,+ hatutakuwa na hatia kuhusiana na kiapo chako ulichotuapisha.” 21 Naye akasema: “Na iwe kama mlivyosema.”
Kwa hiyo akawaruhusu waende zao, nao wakaondoka. Baadaye, akafunga ile kamba nyekundu dirishani. 22 Basi wakaondoka na kuelekea milimani, wakakaa huko kwa siku tatu, mpaka wale waliokuwa wakiwafuatia waliporudi. Waliwatafuta katika kila barabara lakini hawakuwapata. 23 Kisha wapelelezi hao wawili wakaondoka milimani, wakavuka mto na kwenda kwa Yoshua mwana wa Nuni. Wakamsimulia mambo yote yaliyowapata. 24 Halafu wakamwambia hivi Yoshua: “Yehova ametupatia nchi yote.+ Na kwa hakika wakaaji wote wa nchi wamevunjika moyo kwa sababu yetu.”+
3 Ndipo Yoshua na Waisraeli wote* wakaamka asubuhi na mapema na kusafiri kutoka Shitimu+ mpaka Yordani. Wakalala hapo usiku kabla ya kuvuka.
2 Baada ya siku tatu, viongozi+ walipita kambini 3 na kuwaamuru watu, “Mara tu mtakapoliona sanduku la agano la Yehova Mungu wenu likiwa limebebwa na makuhani Walawi,+ mwondoke na kulifuata, 4 ili mjue njia ya kupita kwa kuwa hamjawahi kupita njia hiyo, lakini muwe umbali wa mikono 2,000* hivi kutoka kwenye sanduku hilo; msilikaribie zaidi.”
5 Kisha Yoshua akawaambia watu: “Jitakaseni,+ kwa maana kesho Yehova atafanya mambo yanayostaajabisha kati yenu.”+
6 Halafu Yoshua akawaambia makuhani: “Bebeni sanduku la agano+ na muwatangulie watu.” Basi wakabeba sanduku la agano na kuwatangulia watu.
7 Ndipo Yehova akamwambia Yoshua: “Leo nitaanza kukukweza machoni pa Waisraeli wote,+ ili wajue kwamba nitakuwa pamoja nawe+ kama nilivyokuwa pamoja na Musa.+ 8 Waamuru hivi makuhani wanaobeba sanduku la agano: ‘Mtakapofika kwenye ukingo wa maji ya Yordani, ingieni na kusimama tuli ndani ya maji ya Yordani.’”+
9 Yoshua akawaambia Waisraeli: “Njooni hapa msikilize maneno ya Yehova Mungu wenu.” 10 Kisha Yoshua akasema: “Kwa njia hii mtajua kwamba Mungu aliye hai yumo miongoni mwenu,+ na bila shaka atawafukuza mbele yenu Wakanaani, Wahiti, Wahivi, Waperizi, Wagirgashi, Waamori, na Wayebusi.+ 11 Tazameni! Sanduku la agano la Bwana wa dunia nzima linawatangulia kuingia ndani ya Yordani. 12 Sasa chagueni wanaume 12 kutoka katika makabila ya Israeli, yaani, kila kabila mtu mmoja,+ 13 na mara tu nyayo za makuhani wanaobeba Sanduku la Yehova, Bwana wa dunia nzima, zitakapogusa maji ya Yordani, maji ya Yordani yanayotoka upande wa juu yatasimamishwa, yatakuwa tuli kama bwawa.”*+
14 Basi watu walipotoka ndani ya mahema yao kabla tu ya kuvuka Yordani, makuhani waliobeba sanduku la agano+ wakawatangulia watu. 15 Mara tu makuhani waliobeba lile Sanduku walipofika Yordani na kutumbukiza miguu yao ukingoni mwa mto huo (kwa maana maji ya Yordani hufurika kwenye kingo zake+ sikuzote za mavuno), 16 maji yanayotoka upande wa juu yakaacha kutiririka. Yakasimama tuli kama bwawa* mbali sana huko Adamu, jiji lililo karibu na Sarethani, na yale yanayoshuka kwenye Bahari ya Araba, yaani, Bahari ya Chumvi, yakakauka. Yalisimamishwa, na watu wakavuka kuelekea Yeriko. 17 Makuhani waliobeba sanduku la agano la Yehova wakaendelea kusimama tuli kwenye nchi kavu+ katikati ya Yordani, huku Waisraeli wote wakivuka kwenye nchi kavu+ mpaka taifa lote lilipovuka Yordani.
4 Baada tu ya taifa lote kuvuka Yordani, Yehova akamwambia Yoshua: 2 “Wachukue wanaume 12 kutoka kati ya watu, yaani, mtu mmoja kutoka katika kila kabila,+ 3 na uwaamuru hivi: ‘Chukueni mawe 12 kutoka katikati ya Yordani, mahali ambapo miguu ya makuhani ilisimama tuli,+ myabebe na kuyaweka mahali mtakapolala usiku huu.’”+
4 Basi Yoshua akawaita wale wanaume 12 aliowachagua kutoka kati ya Waisraeli, yaani, mtu mmoja kutoka katika kila kabila; 5 Yoshua akawaambia: “Nendeni katikati ya Yordani mbele ya sanduku la Yehova Mungu wenu, na kila mmoja wenu abebe jiwe begani, kulingana na idadi ya makabila ya Waisraeli, 6 ili yawe ishara kwenu. Ikiwa watoto* wenu watawauliza wakati ujao, ‘Mawe haya ni ya nini?’+ 7 waambieni: ‘Sanduku la agano la Yehova lilipovushwa Yordani, maji ya Yordani yalizuiwa yasitiririke.+ Basi mawe haya yatakuwa kumbukumbu la kudumu kwa Waisraeli.’”+
8 Kwa hiyo Waisraeli wakafanya kama Yoshua alivyowaamuru. Wakachukua mawe 12 kutoka katikati ya Yordani, kama Yehova alivyomwagiza Yoshua, kulingana na idadi ya makabila ya Waisraeli. Wakayapeleka mahali walipolala usiku na kuyaweka hapo.
9 Pia Yoshua akaweka mawe 12 katikati ya Yordani mahali iliposimama miguu ya makuhani waliobeba sanduku la agano,+ na mawe hayo yako huko mpaka leo.
10 Makuhani waliobeba lile Sanduku waliendelea kusimama katikati ya Yordani mpaka watu walipofanya mambo yote ambayo Yehova alimwamuru Yoshua, sawasawa na mambo yote ambayo Musa alikuwa amemwamuru Yoshua. Wakati huohuo, watu waliharakisha kuvuka. 11 Baada tu ya watu wote kuvuka, makuhani waliobeba Sanduku la Yehova wakavuka huku watu wakiwatazama.+ 12 Na watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase wakavuka wakiwa wamejipanga kivita+ na kuwatangulia Waisraeli wengine, kama Musa alivyokuwa amewaagiza.+ 13 Wanajeshi wapatao 40,000 wakiwa na silaha tayari kwa vita wakavuka mbele za Yehova na kuingia katika jangwa tambarare la Yeriko.
14 Siku hiyo Yehova alimkweza Yoshua machoni pa Waisraeli wote,+ wakamheshimu sana* sikuzote za maisha yake, kama walivyomheshimu sana Musa.+
15 Ndipo Yehova akamwambia Yoshua: 16 “Waamuru makuhani wanaobeba sanduku+ la Ushahidi watoke ndani ya Yordani.” 17 Basi Yoshua akawaamuru hivi makuhani: “Tokeni ndani ya Yordani.” 18 Makuhani waliobeba sanduku la agano+ la Yehova walipotoka katikati ya Yordani na nyayo zao kukanyaga nchi kavu, maji ya Yordani yakaanza kutiririka tena na kingo zake zikafurika+ kama mwanzoni.
19 Watu walivuka Yordani siku ya kumi ya mwezi wa kwanza na kupiga kambi Gilgali+ kwenye mpaka wa mashariki wa Yeriko.
20 Kisha Yoshua akapanga kule Gilgali yale mawe 12 ambayo walichukua kutoka Mto Yordani.+ 21 Akawaambia hivi Waisraeli: “Watoto wenu watakapowauliza wakati ujao, ‘Mawe haya ni ya nini?’+ 22 Waambieni, ‘Waisraeli walivuka katikati ya Mto Yordani kwenye nchi kavu+ 23 Yehova Mungu wenu alipoyakausha maji ya Yordani mbele yao mpaka walipovuka, kama Yehova Mungu wenu alivyoikausha Bahari Nyekundu* mbele yetu mpaka tulipovuka.+ 24 Alifanya hivyo ili watu wote duniani wajue jinsi mkono wa Yehova ulivyo na nguvu+ na ili ninyi mmwogope Yehova Mungu wenu sikuzote.’”
5 Mara tu wafalme wote wa Waamori+ waliokuwa upande wa magharibi* wa Yordani na wafalme wote wa Wakanaani+ waliokuwa karibu na bahari waliposikia kwamba Yehova alikausha maji ya Yordani mpaka Waisraeli walipovuka, wakafa moyo*+ na hawakuwa na ujasiri wowote kwa sababu ya Waisraeli.+
2 Wakati huo Yehova akamwambia hivi Yoshua: “Tengeneza visu vya jiwe gumu na uwatahiri+ wanaume Waisraeli tena, mara ya pili.” 3 Basi Yoshua akatengeneza visu vya jiwe gumu na kuwatahiri wanaume Waisraeli kule Gibeath-haaralothi.*+ 4 Yoshua aliwatahiri kwa sababu wanaume wote waliotoka Misri, yaani, wanaume wote wa kwenda vitani,* walikufa nyikani walipotoka Misri.+ 5 Kwa maana watu wote waliotoka Misri walikuwa wametahiriwa, lakini watu wote waliozaliwa nyikani wakiwa safarini kutoka Misri hawakuwa wametahiriwa. 6 Waisraeli walitembea miaka 40+ nyikani mpaka taifa lote lilipokufa, yaani, wanaume wote wa kwenda vitani waliotoka Misri ambao hawakutii sauti ya Yehova.+ Yehova aliwaapia kwamba hatawaruhusu kamwe waione nchi+ ambayo Yehova alikuwa amewaapia mababu zao kwamba atatupatia,+ nchi inayotiririka maziwa na asali.+ 7 Kwa hiyo, akawainua wana wao badala yao.+ Yoshua akawatahiri wana hao kwa sababu hawakuwa wametahiriwa safarini.
8 Walipomaliza kutahiri taifa lote, wakaendelea kukaa kambini mpaka walipopona.
9 Kisha Yehova akamwambia Yoshua: “Leo nimewaondolea aibu ya Misri.” Basi tangu wakati huo mahali hapo panaitwa Gilgali.*+
10 Waisraeli wakaendelea kupiga kambi Gilgali, nao wakaadhimisha Pasaka siku ya 14 ya mwezi huo,+ wakati wa jioni, katika jangwa tambarare la Yeriko. 11 Kesho yake, baada ya Pasaka, siku hiyohiyo wakaanza kula mazao ya nchi, yaani, mikate isiyo na chachu+ na nafaka zilizokaangwa. 12 Mana ilikoma siku iliyofuata, baada ya Waisraeli kula baadhi ya mazao ya nchi; Waisraeli hawakupata mana tena,+ wakaanza kula mazao ya nchi ya Kanaani mwaka huo.+
13 Yoshua alipokuwa karibu na Yeriko, aliinua macho na kumwona mwanamume+ fulani amesimama mbele yake akiwa ameshika upanga uliochomolewa.+ Yoshua akamkaribia na kumuuliza: “Uko upande wetu au wa maadui wetu?” 14 Akamjibu: “Hapana, mimi ni mkuu* wa jeshi la Yehova.”+ Basi Yoshua akaanguka chini kifudifudi, akasujudu, na kumwambia: “Bwana wangu una ujumbe gani kwangu mimi mtumishi wako?” 15 Mkuu wa jeshi la Yehova akamjibu hivi Yoshua: “Vua viatu vyako, kwa sababu mahali unaposimama ni patakatifu.” Yoshua akavua mara moja.+
6 Basi malango ya jiji la Yeriko yalikuwa yamefungwa kabisa kwa sababu ya Waisraeli; hakuna mtu yeyote aliyetoka wala kuingia.+
2 Yehova akamwambia Yoshua, “Tazama, nimetia mikononi mwako Yeriko, mfalme wake, na mashujaa wake hodari.+ 3 Ninyi nyote wanaume wa vita mnapaswa kulizunguka jiji hili, lizungukeni mara moja kwa siku. Mtafanya hivyo kwa siku sita. 4 Waagize makuhani saba wabebe pembe saba za kondoo dume na kulitangulia Sanduku. Lakini siku ya saba, mnapaswa kulizunguka jiji mara saba na makuhani watapiga pembe hizo.+ 5 Pembe za kondoo dume zitakapopigwa, na mara tu mtakaposikia mlio wake,* watu wote watapiga kelele kubwa za vita. Kisha ukuta wa jiji utaanguka chini,+ na kila mtu ataingia jijini moja kwa moja.”
6 Basi Yoshua mwana wa Nuni akawaita makuhani na kuwaambia: “Bebeni sanduku la agano, na makuhani saba wabebe pembe saba za kondoo dume na kulitangulia Sanduku la Yehova.”+ 7 Kisha akawaambia watu, “Nendeni mzunguke jiji, na wanajeshi wenye silaha+ walitangulie Sanduku la Yehova.” 8 Watu wakafanya kama Yoshua alivyowaambia, makuhani saba waliobeba pembe saba za kondoo dume mbele za Yehova, wakatangulia na kupiga pembe hizo, na sanduku la agano la Yehova lilikuwa likiwafuata. 9 Na wanajeshi wenye silaha waliwatangulia makuhani waliokuwa wakizipiga pembe, na walinzi wa nyuma walilifuata Sanduku huku pembe zikipigwa mfululizo.
10 Yoshua alikuwa amewaamuru hivi watu: “Msipige kelele wala kupaza sauti. Msiseme neno lolote mpaka siku nitakapowaambia, ‘Pazeni sauti!’ Ndipo mtakapopaza sauti.” 11 Akaagiza Sanduku la Yehova lipelekwe kuzunguka jiji mara moja, kisha wakarudi kambini na kulala humo usiku.
12 Asubuhi iliyofuata, Yoshua akaamka mapema, na makuhani wakalibeba Sanduku+ la Yehova, 13 makuhani saba waliobeba pembe saba za kondoo dume walilitangulia Sanduku la Yehova wakipiga pembe hizo mfululizo. Nao wanajeshi wenye silaha walitembea mbele yao na walinzi wa nyuma walilifuata Sanduku la Yehova huku pembe zikipigwa mfululizo. 14 Siku ya pili, walilizunguka jiji mara moja, kisha wakarudi kambini. Walifanya hivyo kwa siku sita.+
15 Siku ya saba wakaamka asubuhi na mapema, wakalizunguka jiji kama kawaida. Ni siku hiyo peke yake ambayo walilizunguka jiji mara saba.+ 16 Na mara ya saba, makuhani walipiga pembe na Yoshua akawaambia watu: “Pazeni sauti,+ kwa kuwa Yehova amewapa jiji hili! 17 Jiji na vitu vyote vilivyomo vinapaswa kuharibiwa;+ vyote ni vya Yehova. Ila msimwangamize Rahabu+ yule kahaba na wote walio pamoja naye nyumbani mwake, kwa sababu aliwaficha wajumbe tuliowatuma.+ 18 Lakini mjiepushe na kitu chochote kinachopaswa kuharibiwa,+ ili msikitamani kitu kinachopaswa kuharibiwa na kukichukua,+ msije mkaleta msiba* kwenye kambi ya Waisraeli.+ 19 Lakini fedha yote na dhahabu na vitu vya shaba na chuma ni vitakatifu kwa Yehova.+ Vinapaswa kupelekwa katika hazina ya Yehova.”+
20 Basi watu wakapaza sauti pembe zilipopigwa.+ Na mara tu watu waliposikia sauti za pembe na kupiga kelele kubwa za vita, ukuta ukaanguka chini.+ Kisha kila mtu akaingia jijini moja kwa moja, nao wakaliteka. 21 Wakaangamiza kwa upanga kila kiumbe kilichokuwa jijini, wanaume na wanawake, vijana na wazee, ng’ombe dume, kondoo, na punda.+
22 Yoshua akawaambia wale wanaume wawili waliokuwa wameipeleleza nchi: “Nendeni katika nyumba ya yule mwanamke kahaba, mkamtoe nje pamoja na watu wake wote, kama mlivyomwapia.”+ 23 Basi wale vijana wapelelezi wakaenda kumtoa Rahabu, baba yake, mama yake, ndugu zake, na watu wote wa nyumba yake; naam, wakaitoa nje familia yake yote,+ na kuileta salama salimini nje ya kambi ya Waisraeli.
24 Kisha wakaliteketeza jiji pamoja na kila kitu kilichokuwemo. Lakini fedha, dhahabu, na vitu vya shaba na chuma, wakaviweka katika hazina ya nyumba ya Yehova.+ 25 Yoshua hakumwangamiza Rahabu yule kahaba, watu wa nyumba ya baba yake, na familia yake yote;+ Rahabu anakaa katika Israeli mpaka leo,+ kwa sababu aliwaficha wajumbe waliotumwa na Yoshua kupeleleza Yeriko.+
26 Wakati huo Yoshua alitangaza kiapo* hiki: “Na alaaniwe mbele za Yehova mtu atakayejaribu kulijenga tena jiji hili la Yeriko. Atakapojenga msingi wake, mzaliwa wake wa kwanza atakufa, na atakapoweka malango yake, mwana wake wa mwisho atakufa.”+
27 Basi Yehova alikuwa pamoja na Yoshua,+ na umaarufu wake ukaenea duniani pote.+
7 Lakini Waisraeli walikosa uaminifu kuhusiana na vitu vilivyopaswa kuharibiwa, kwa kuwa Akani+ mwana wa Karmi, mwana wa Zabdi, mwana wa Zera, wa kabila la Yuda, alichukua baadhi ya vitu vilivyopaswa kuharibiwa.+ Ndipo hasira ya Yehova ikawaka dhidi ya Waisraeli.+
2 Basi Yoshua akatuma wanaume kutoka Yeriko waende Ai,+ karibu na Beth-aveni, upande wa mashariki wa Betheli,+ akawaambia: “Pandeni mkaipeleleze nchi.” Kwa hiyo wanaume hao wakapanda na kwenda kupeleleza jiji la Ai. 3 Waliporudi kwa Yoshua, wakamwambia: “Si lazima watu wote waende. Wanaume elfu mbili au elfu tatu hivi wanatosha kulishinda jiji la Ai. Usiwachoshe watu wote kwa kuwatuma huko, kwa sababu jiji hilo lina watu wachache tu.”
4 Basi wanaume wapatao 3,000 wakapanda huko, lakini wakakimbizwa na wanaume wa Ai.+ 5 Na wanaume hao wa Ai wakawaua watu 36, wakawakimbiza kutoka nje ya lango la jiji mpaka Shebarimu,* wakaendelea kuwaua kwenye mteremko. Basi ujasiri wa watu ukayeyuka* na kuwa kama maji.
6 Ndipo Yoshua akararua mavazi yake na kuanguka chini kifudifudi mbele ya Sanduku la Yehova mpaka jioni, yeye pamoja na wazee wa Israeli, nao wakaendelea kujirushia mavumbi vichwani. 7 Yoshua akasema: “Ole wangu, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, kwa nini umewaleta watu hawa njia yote hii na kuwavusha Yordani ili tu kututia mikononi mwa Waamori watuangamize? Ni afadhali tungeridhika kubaki ng’ambo ile nyingine ya* Yordani! 8 Nakusihi Ee Yehova, niseme nini baada ya Waisraeli kuwakimbia maadui wao? 9 Wakanaani na wakaaji wote wa nchi hii watakaposikia habari hii, watatuzingira na kufutilia mbali jina letu kutoka duniani, nawe utafanya nini kwa ajili ya jina lako kuu?”+
10 Yehova akamwambia Yoshua: “Inuka! Kwa nini umelala chini kifudifudi? 11 Waisraeli wametenda dhambi. Wamevunja agano langu+ nililowaamuru washike. Wamechukua baadhi ya vitu vilivyopaswa kuharibiwa,+ wameviiba+ na kuvificha kati ya vitu vyao.+ 12 Kwa hiyo, Waisraeli hawawezi kusimama dhidi ya maadui wao. Watageuka na kuwakimbia maadui wao, kwa sababu wanapaswa kuangamizwa. Sitakuwa pamoja nanyi tena msipoharibu kitu mlicho nacho kinachopaswa kuharibiwa.+ 13 Inuka uwatakase watu!+ Waambie, ‘Jitakaseni kesho, kwa sababu Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: “Kuna kitu kinachopaswa kuharibiwa miongoni mwenu, Ee Israeli. Hamtaweza kusimama dhidi ya maadui wenu msipoondoa kitu kinachopaswa kuharibiwa. 14 Mtakusanyika asubuhi, kabila kwa kabila, na kabila ambalo Yehova atachagua+ litakaribia, ukoo kwa ukoo, na ukoo ambao Yehova atachagua utakaribia, nyumba kwa nyumba, na nyumba ambayo Yehova atachagua itakaribia, mwanamume kwa mwanamume. 15 Mtu atakayepatikana akiwa na kitu kinachopaswa kuharibiwa atateketezwa kwa moto,+ yeye pamoja na vitu vyake vyote, kwa sababu amevunja agano+ la Yehova na kwa sababu ametenda jambo la aibu katika Israeli.”’”
16 Kesho yake, Yoshua akaamka asubuhi na mapema akawakusanya Waisraeli, kabila kwa kabila, na kabila la Yuda likachaguliwa. 17 Kisha akaleta karibu koo za Yuda na ukoo wa Wazera+ ukachaguliwa, kisha akaleta karibu familia za ukoo wa Wazera, mwanamume kwa mwanamume, na Zabdi akachaguliwa. 18 Mwishowe akaleta karibu familia ya Zabdi, mwanamume kwa mwanamume, naye Akani mwana wa Karmi, mwana wa Zabdi, mwana wa Zera, wa kabila la Yuda, akachaguliwa.+ 19 Kisha Yoshua akamwambia Akani: “Tafadhali mwanangu, mheshimu Yehova Mungu wa Israeli na uungame kwake. Tafadhali niambie jambo ulilofanya. Usinifiche chochote.”
20 Akani akamwambia Yoshua: “Kwa kweli ni mimi niliyemtendea dhambi Yehova Mungu wa Israeli, na hili ndilo jambo nililofanya. 21 Nilipoona katika nyara vazi rasmi maridadi kutoka Shinari+ na shekeli 200 za fedha na kipande kimoja cha dhahabu chenye uzito wa shekeli 50,* nilivitamani, kwa hiyo nikavichukua. Nimevificha ardhini ndani ya hema langu, na fedha ziko chini yake.”
22 Mara moja Yoshua akatuma wajumbe, wakakimbia kwenda hemani, wakakuta lile vazi likiwa limefichwa ndani ya hema lake, na fedha zilikuwa chini yake. 23 Basi wakavichukua vitu hivyo kutoka hemani na kumletea Yoshua na Waisraeli wote na kuviweka mbele za Yehova. 24 Yoshua na Waisraeli wote wakamchukua Akani+ mwana wa Zera, zile fedha, lile vazi rasmi maridadi, na kile kipande cha dhahabu,+ pamoja na wanawe, binti zake, ng’ombe dume wake, punda wake, kondoo na mbuzi wake, hema lake, na vitu vyake vyote, wakavileta katika Bonde la* Akori.+ 25 Yoshua akasema: “Kwa nini umetuletea msiba?*+ Leo Yehova atakuletea msiba.” Ndipo Waisraeli wote wakawapiga mawe,+ kisha wakawateketeza kwa moto.+ Naam, waliwapiga mawe wote. 26 Nao wakarundika mawe mengi juu yake ambayo yapo hadi leo. Ndipo hasira ya Yehova ikapoa.+ Ndiyo sababu tangu siku hiyo mahali hapo panaitwa Bonde la Akori.*
8 Kisha Yehova akamwambia Yoshua: “Usiogope wala usihofu.+ Nenda na wanajeshi wote ulishambulie jiji la Ai. Naam, nimemtia mikononi mwako mfalme wa Ai, watu wake, jiji lake, na nchi yake.+ 2 Mlitendee Ai na mfalme wake kama mlivyolitendea Yeriko na mfalme wake,+ lakini mnaweza kujichukulia nyara zake na mifugo yake. Wekeni watu watakaovizia nyuma ya jiji hilo.”
3 Basi Yoshua na wanajeshi wote wakaenda kulishambulia jiji la Ai. Yoshua akachagua mashujaa hodari 30,000 na kuwatuma wakati wa usiku. 4 Akawaamuru hivi: “Mtavizia nyuma ya jiji. Msiende mbali sana na jiji, na nyote kaeni tayari. 5 Mimi na watu walio pamoja nami tutalikaribia jiji, na watakapotoka ili kutushambulia kama walivyofanya mwanzoni,+ tutawakimbia. 6 Watakapotukimbiza, tutawavuta mbali na jiji lao, kwa kuwa watasema, ‘Wanatukimbia kama walivyofanya mwanzoni.’+ Nasi tutaendelea kuwakimbia. 7 Kisha mtatoka mahali mnapovizia na kuliteka jiji; Yehova Mungu wenu atalitia mikononi mwenu. 8 Na mara tu baada ya kuliteka jiji, mnapaswa kuliteketeza kwa moto.+ Mtafanya kama Yehova alivyoagiza. Hayo ndiyo maagizo mtakayofuata.”
9 Kisha Yoshua akawatuma, nao wakaenda kuvizia; wakapiga kambi kati ya Betheli na Ai, upande wa magharibi wa Ai, lakini Yoshua alikaa pamoja na watu usiku huo.
10 Yoshua akaamka asubuhi na mapema, akakusanya wanajeshi, kisha yeye na wazee wa Israeli wakawaongoza hadi Ai. 11 Na wanajeshi wote+ waliokuwa pamoja naye wakapanda na kukaribia mbele ya jiji. Wakapiga kambi upande wa kaskazini wa Ai, na bonde lilikuwa kati yao na Ai. 12 Wakati huo, alikuwa ameweka wanajeshi wapatao 5,000 wavizie+ kati ya Betheli+ na Ai, upande wa magharibi wa jiji. 13 Basi kikosi kikubwa kilikuwa upande wa kaskazini wa jiji+ na wanajeshi waliokuwa wakivizia nyuma walikuwa upande wa magharibi wa jiji,+ na usiku huo Yoshua akaenda katikati ya bonde.*
14 Na mara tu mfalme wa Ai alipoona hilo, yeye pamoja na wanaume wa jiji wakaamka mapema na kwenda haraka kupigana na Waisraeli mahali fulani ng’ambo ya jangwa tambarare. Lakini hakujua kwamba kulikuwa na wanajeshi waliokuwa wakivizia nyuma ya jiji. 15 Watu wa Ai walipowashambulia, Yoshua na wanajeshi wote Waisraeli wakakimbia barabarani kuelekea nyikani.+ 16 Ndipo watu wote waliokuwa ndani ya jiji wakaambiwa wawakimbize; na walipokuwa wakimkimbiza Yoshua, walienda mbali na jiji. 17 Hakuna mwanamume yeyote aliyebaki Ai na Betheli, wote waliwakimbiza Waisraeli. Waliacha jiji lao wazi na kuwakimbiza Waisraeli.
18 Sasa Yehova akamwambia Yoshua, “Nyoosha mkuki ulio mkononi mwako kuelekea Ai,+ kwa maana nitalitia jiji hilo mikononi mwako.”+ Basi Yoshua akanyoosha mkuki uliokuwa mkononi mwake kuelekea jiji hilo. 19 Na mara tu aliponyoosha mkono wake, wanajeshi waliokuwa wakivizia wakatoka haraka mahali walipokuwa, wakakimbia kuingia jijini, na kuliteka jiji hilo. Na mara moja wakaliteketeza.+
20 Wanaume wa Ai walipogeuka na kuangalia nyuma, wakaona moshi ukipanda angani kutoka jijini, wakaishiwa na nguvu na hawakuweza kukimbia upande wowote. Kisha wanajeshi Waisraeli waliokuwa wakikimbia kuelekea nyikani wakageuka na kuanza kuwashambulia wale waliokuwa wakiwakimbiza. 21 Yoshua na Waisraeli wote walipoona kwamba wanajeshi waliovizia walikuwa wameliteka jiji na kuona moshi ukipanda kutoka jijini, wakageuka na kuwashambulia wanaume wa Ai. 22 Na wale walioliteka jiji wakaenda kuungana na wenzao, na wanaume wa Ai wakanaswa katikati, baadhi ya Waisraeli walikuwa upande huu na wengine upande wa pili, wakawaua na hakuna yeyote aliyeokoka wala kuponyoka.+ 23 Lakini walimkamata mfalme wa Ai+ akiwa hai na kumpeleka kwa Yoshua.
24 Baada ya Waisraeli kumaliza kuwaua wakaaji wote wa Ai nyikani, ambako waliwafuatia na kumuua kila mmoja wao kwa upanga, Waisraeli wote walirudi Ai na kuwaua kwa upanga watu waliobaki jijini. 25 Watu wote walioangamia siku hiyo, wanaume na wanawake, walikuwa 12,000, yaani, watu wote wa Ai. 26 Yoshua hakuushusha mkono wake uliokuwa umeshika mkuki+ mpaka alipowaangamiza wakaaji wote wa Ai.+ 27 Hata hivyo, Waisraeli walijichukulia mifugo na nyara za jiji kama Yehova alivyomwagiza Yoshua.+
28 Kisha Yoshua akateketeza jiji la Ai, na tangu siku hiyo likabaki rundo la kudumu la magofu.+ 29 Akamtundika mtini mfalme wa Ai mpaka jioni, na jua lilipokaribia kutua, Yoshua akaagiza maiti yake iondolewe mtini.+ Kisha wakaitupa kwenye lango la jiji na kurundika mawe mengi juu ya maiti hiyo, na rundo hilo lipo mpaka leo.
30 Kisha Yoshua akamjengea Yehova Mungu wa Israeli madhabahu kwenye Mlima Ebali,+ 31 kama Musa mtumishi wa Yehova alivyowaamuru Waisraeli na kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Sheria+ ya Musa: “Madhabahu ya mawe ambayo hayakuchongwa wala kuguswa na kifaa chochote cha chuma.”+ Na juu yake wakamtolea Yehova dhabihu za kuteketezwa na pia dhabihu za ushirika.+
32 Kisha akiwa huko akaandika juu ya mawe hayo nakala ya Sheria+ ambayo Musa alikuwa ameandika mbele ya Waisraeli.+ 33 Waisraeli wote pamoja na wazee wao, viongozi wao, na waamuzi wao, walikuwa wamesimama pande mbili za hilo sanduku la agano la Yehova mbele ya makuhani Walawi waliokuwa wamelibeba. Wakaaji wageni na pia wenyeji walikuwepo.+ Nusu yao walisimama mbele ya Mlima Gerizimu, na nusu walisimama mbele ya Mlima Ebali+ (kama Musa mtumishi wa Yehova alivyokuwa ameagiza mwanzoni),+ ili kuwabariki Waisraeli. 34 Kisha Yoshua akasoma kwa sauti maneno yote ya Sheria,+ baraka+ na laana,+ kulingana na yote ambayo yameandikwa katika kitabu cha Sheria. 35 Hakuna neno lolote kati ya maneno yote ambayo Musa alikuwa ameamuru ambalo Yoshua hakusoma kwa sauti mbele ya kutaniko lote la Israeli,+ lililotia ndani wanawake, watoto, na wakaaji wageni+ walioishi* miongoni mwao.+
9 Waliposikia habari hizo, wafalme wote waliokuwa upande wa magharibi wa Yordani,+ katika eneo lenye milima, na Shefela, na eneo lote la pwani ya Bahari Kuu,*+ na mbele ya Lebanoni—Wahiti, Waamori, Wakanaani, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi+— 2 wakaungana ili kupigana na Yoshua na Waisraeli.+
3 Wakaaji wa Gibeoni+ walisikia pia mambo ambayo Yoshua alitenda katika jiji la Yeriko+ na Ai.+ 4 Basi wakatenda kwa busara na kuweka vyakula katika magunia yaliyochakaa na kuyabeba kwa punda wao, pamoja na viriba vya divai vilivyochakaa na kutiwa viraka; 5 pia walivaa viatu vilivyochakaa vyenye viraka na nguo zilizochakaa. Na mikate waliyobeba ilikuwa imekauka na kuvunjika-vunjika. 6 Kisha wakaenda kwa Yoshua kambini kule Gilgali,+ wakamwambia yeye na wazee wa Waisraeli: “Tumetoka nchi ya mbali. Basi fanyeni agano pamoja nasi.” 7 Lakini wazee wa Waisraeli wakawaambia hao Wahivi:+ “Huenda mnakaa karibu nasi. Tunawezaje kufanya agano nanyi?”+ 8 Wakamjibu Yoshua: “Sisi ni watumishi* wako.”
Kisha Yoshua akawauliza: “Ninyi ni nani, na mnatoka wapi?” 9 Wakamjibu: “Sisi watumishi wako tumetoka nchi ya mbali sana+ kwa sababu ya heshima ya jina la Yehova Mungu wako, kwa kuwa tumesikia umaarufu wake na mambo yote aliyotenda Misri+ 10 na mambo yote aliyowatendea wale wafalme wawili wa Waamori waliokuwa ng’ambo ya* Yordani, yaani, Mfalme Sihoni+ wa Heshboni na Mfalme Ogu+ wa Bashani, aliyekuwa Ashtarothi. 11 Kwa hiyo wazee wetu na wakaaji wote wa nchi yetu wakatuambia, ‘Bebeni chakula kwa ajili ya safari mwende mkakutane nao. Waambieni hivi: “Tutakuwa watumishi wenu;+ basi fanyeni agano pamoja nasi.”’+ 12 Mikate hii ilikuwa moto tulipotoka nyumbani ili kuja hapa. Sasa angalieni jinsi ilivyokauka na inavyovunjika-vunjika.+ 13 Na viriba hivi vilikuwa vipya tulipovijaza divai, lakini sasa vimepasuka.+ Na nguo na viatu vyetu vimechakaa kwa sababu ya safari ndefu.”
14 Ndipo wazee wa Waisraeli wakachukua* vyakula vyao, lakini hawakutafuta mwongozo wa Yehova.+ 15 Basi Yoshua akafanya amani nao,+ pia akafanya agano pamoja nao ili kuwaacha waishi, na hivyo ndivyo wakuu wa Waisraeli walivyowaapia.+
16 Siku tatu baada ya kufanya agano pamoja nao, wakasikia kwamba walikuwa majirani wao na waliishi karibu nao. 17 Ndipo Waisraeli wakaanza safari na kufika katika majiji ya watu hao siku ya tatu; na majiji yao yalikuwa Gibeoni,+ Kefira, Beerothi, na Kiriath-yearimu.+ 18 Lakini Waisraeli hawakuwashambulia, kwa sababu wakuu wa Waisraeli walikuwa wamewaapia kwa jina la Yehova+ Mungu wa Israeli. Kwa hiyo Waisraeli wote wakaanza kuwanung’unikia wakuu hao. 19 Basi wakuu wote wakawaambia hivi: “Kwa kuwa tuliwaapia kwa jina la Yehova Mungu wa Israeli haturuhusiwi kuwadhuru. 20 Hili ndilo jambo tutakalofanya: Tutawaacha waishi, ili hasira ya Mungu isiwake dhidi yetu kwa sababu ya kiapo tulichowaapia.”+ 21 Wakuu wakaendelea kuwaambia hivi: “Waacheni waishi, lakini watakuwa wakusanyaji wa kuni na watekaji wa maji kwa ajili ya Waisraeli wote.” Hivyo ndivyo wakuu walivyowaahidi.
22 Basi Yoshua akawaita na kuwauliza: “Kwa nini mlitudanganya mkisema, ‘Tumetoka mbali sana,’ na kumbe mnaishi karibu kabisa nasi?+ 23 Kuanzia sasa mmelaaniwa,+ na sikuzote mtakuwa watumwa wa kukusanya kuni na kuteka maji kwa ajili ya nyumba ya Mungu wangu.” 24 Ndipo wakamjibu Yoshua: “Tulifanya hivyo kwa sababu sisi watumishi wako tuliambiwa waziwazi kwamba Yehova Mungu wako alimwamuru Musa mtumishi wake awape ninyi nchi yote na kuwaangamiza wakaaji wote kutoka mbele yenu.+ Basi tulifanya hivyo kwa sababu tuliogopa mtatuua.+ 25 Sasa tuonyeshe rehema.* Tutendee upendavyo.” 26 Na hivyo ndivyo alivyofanya; aliwaokoa kutoka mikononi mwa Waisraeli, nao hawakuwaua. 27 Lakini tangu siku hiyo, Yoshua akawafanya kuwa wakusanyaji wa kuni na watekaji wa maji kwa ajili ya kusanyiko+ na kwa ajili ya madhabahu ya Yehova mahali ambapo Mungu angechagua.+
10 Mara tu Mfalme Adoni-sedeki wa Yerusalemu aliposikia kwamba Yoshua ameteka Ai na kuliangamiza, na kulitendea Ai na mfalme wake+ kama alivyolitendea Yeriko na mfalme wake,+ na jinsi wakaaji wa Gibeoni walivyofanya amani na Waisraeli+ na kuendelea kukaa kati yao, 2 akaogopa sana,+ kwa sababu Gibeoni lilikuwa jiji kubwa kama majiji yaliyotawaliwa na mfalme. Lilikuwa kubwa kuliko Ai,+ na wanaume wake wote walikuwa mashujaa. 3 Basi Adoni-sedeki mfalme wa Yerusalemu akatuma ujumbe huu kwa Hohamu mfalme wa Hebroni,+ Piramu mfalme wa Yarmuthi, Yafia mfalme wa Lakishi, na kwa Debiri mfalme wa Egloni:+ 4 “Njooni mnisaidie kuwashambulia wakaaji wa Gibeoni, kwa sababu wamefanya amani na Yoshua na Waisraeli.”+ 5 Ndipo wafalme watano wa Waamori,+ yaani, mfalme wa Yerusalemu, mfalme wa Hebroni, mfalme wa Yarmuthi, mfalme wa Lakishi, na mfalme wa Egloni wakakusanyika pamoja na majeshi yao, wakaenda kupiga kambi ili kulishambulia jiji la Gibeoni.
6 Kisha wazee wa Gibeoni wakatuma ujumbe kwa Yoshua kambini Gilgali,+ wakisema: “Usituache* sisi watumwa wako.+ Njoo haraka ili utuokoe na kutusaidia! Wafalme wote wa Waamori kutoka katika eneo lenye milima wamekusanyika ili kutushambulia.” 7 Basi Yoshua akapanda kutoka Gilgali pamoja na jeshi lake lote na mashujaa hodari.+
8 Ndipo Yehova akamwambia Yoshua: “Usiwaogope,+ kwa maana nimewatia mikononi mwako.+ Hakuna mtu yeyote kati yao atakayekushinda.”+ 9 Yoshua akawashambulia ghafla baada ya kutembea usiku kucha kutoka Gilgali. 10 Yehova akawavuruga,+ na Waisraeli wakawaangamiza wengi wao kule Gibeoni, wakawafuatia kwenye njia inayopanda kwenda Beth-horoni na kuwaua mpaka Azeka na Makeda. 11 Walipokuwa wakiwakimbia Waisraeli, Yehova akawanyeshea mvua ya mawe makubwa kutoka angani kwenye mteremko wa Beth-horoni mpaka Azeka, nao wakafa. Kwa kweli, wale waliouawa na mvua ya mawe walikuwa wengi kuliko wale waliouawa na Waisraeli kwa upanga.
12 Ni siku hiyo, siku ambayo Yehova aliwashinda kabisa Waamori mbele ya Waisraeli, ndipo Yoshua alipomwambia hivi Yehova mbele ya Waisraeli:
13 Basi jua likasimama tuli na mwezi ukatulia mpaka taifa la Israeli lilipolipiza kisasi dhidi ya maadui wake. Je, haijaandikwa hivi katika kitabu cha Yashari:+ Jua lilisimama tuli katikati ya mbingu na halikutua kwa siku nzima? 14 Haijawahi kamwe kutokea siku kama hiyo, kabla au baada yake, ambayo Yehova aliisikiliza sauti ya mwanadamu+ katika njia hiyo, kwa sababu Yehova alikuwa akiwapigania Waisraeli.+
15 Baada ya mambo hayo Yoshua na Waisraeli wote wakarudi kambini Gilgali.+
16 Wakati huo, wale wafalme watano walikimbia na kujificha pangoni kule Makeda.+ 17 Yoshua akaambiwa: “Wale wafalme watano wamejificha pangoni kule Makeda.”+ 18 Basi Yoshua akasema: “Bingirisheni mawe makubwa kwenye mwingilio wa pango hilo na kuweka walinzi hapo. 19 Lakini ninyi wengine msikae hapo. Wakimbizeni maadui wenu na kuwashambulia kutokea nyuma.+ Msiwape nafasi ya kuingia katika majiji yao, kwa kuwa Yehova Mungu wenu amewatia mikononi mwenu.”
20 Baada ya Yoshua na Waisraeli kuwaangamiza karibu watu wote na wachache waliobaki kukimbilia katika majiji yenye ngome, 21 Waisraeli wote wakarudi salama kambini kwa Yoshua kule Makeda. Hakuna mtu aliyethubutu kusema neno lolote* dhidi ya Waisraeli. 22 Kisha Yoshua akasema, “Fungueni mwingilio wa pango, watoeni nje wale wafalme watano na kuwaleta kwangu.” 23 Basi wakawatoa pangoni wafalme hawa watano na kuwaleta kwake: mfalme wa Yerusalemu, mfalme wa Hebroni, mfalme wa Yarmuthi, mfalme wa Lakishi, na mfalme wa Egloni.+ 24 Walipomletea Yoshua wafalme hao, akawaita wanaume wote wa Israeli na kuwaambia makamanda wa jeshi walioenda naye: “Njooni. Wakanyageni nyuma ya shingo wafalme hawa.” Basi wakaja na kuwakanyaga nyuma ya shingo.+ 25 Ndipo Yoshua akawaambia: “Msiogope wala msihofu.+ Iweni jasiri na imara, kwa maana hivi ndivyo Yehova atakavyowatendea maadui wenu wote ambao mnapigana nao.”+
26 Kisha Yoshua akawapiga na kuwaua, akawatundika juu ya miti mitano, wakaning’inia juu ya miti hiyo mpaka jioni. 27 Na jua lilipotua, Yoshua akaagiza washushwe kutoka kwenye miti+ hiyo na kutupwa ndani ya pango ambamo walikuwa wamejificha. Kisha mawe makubwa yakawekwa kwenye mwingilio wa pango hilo, nayo yapo mpaka leo.
28 Yoshua akateka jiji la Makeda+ siku hiyo na kuwaangamiza wakaaji wake kwa upanga. Akamwangamiza mfalme wake na wakaaji wote, na hakuna mtu yeyote aliyebaki.*+ Alimtendea mfalme wa Makeda+ kama alivyomtendea mfalme wa Yeriko.
29 Kisha Yoshua na Waisraeli wote wakatoka Makeda na kwenda Libna, wakalishambulia jiji la Libna.+ 30 Yehova akalitia pia jiji hilo na mfalme wake+ mikononi mwa Waisraeli, wakalishambulia na kuwaangamiza wakaaji wote kwa upanga, na hakuna yeyote aliyebaki humo. Wakamtendea mfalme wake kama walivyomtendea mfalme wa Yeriko.+
31 Kisha Yoshua na Waisraeli wote wakatoka Libna na kwenda Lakishi,+ wakapiga kambi huko na kulishambulia. 32 Yehova akalitia jiji la Lakishi mikononi mwa Waisraeli, nao wakaliteka siku ya pili. Wakalishambulia na kuwaangamiza wakaaji wote* kwa upanga,+ kama walivyofanya kule Libna.
33 Ndipo Horamu mfalme wa Gezeri+ akaenda kulisaidia Lakishi, lakini Yoshua akamuua yeye na watu wake wote, na hakuna yeyote aliyebaki.
34 Kutoka Lakishi, Yoshua na Waisraeli wote wakaenda Egloni,+ wakapiga kambi huko na kulishambulia. 35 Wakaliteka siku hiyo na kuliangamiza kwa upanga. Wakawaangamiza wakaaji wote siku hiyo, kama walivyofanya kule Lakishi.+
36 Kutoka Egloni, Yoshua na Waisraeli wote wakaenda Hebroni+ na kulishambulia. 37 Wakaliteka na kuliangamiza kwa upanga jiji hilo, mfalme wake, miji yake, na wakaaji wote, na hakuna yeyote aliyebaki. Yoshua aliliangamiza pamoja na wakaaji wote,* kama alivyofanya kule Egloni.
38 Mwishowe Yoshua na Waisraeli wote wakaelekea Debiri+ na kulishambulia. 39 Akaliteka pamoja na mfalme wake, na miji yake yote, wakawaangamiza wakaaji wote kwa upanga,+ na hakuna yeyote aliyebaki.+ Alilitendea Debiri na mfalme wake kama alivyolitendea Hebroni na pia Libna na mfalme wake.
40 Hivyo Yoshua akaiteka nchi yote kutia ndani eneo lenye milima, Negebu, Shefela,+ na miteremko, na kuwashinda wafalme wao wote, na hakuna yeyote aliyebaki; alimwangamiza kila kiumbe anayepumua,+ kama Yehova Mungu wa Israeli alivyoamuru.+ 41 Yoshua aliwashinda kuanzia Kadesh-barnea+ mpaka Gaza+ na nchi yote ya Gosheni+ kufika Gibeoni.+ 42 Yoshua aliwateka wafalme hao wote na nchi zao kwa wakati mmoja, kwa sababu Yehova Mungu wa Israeli alikuwa akiwapigania Waisraeli.+ 43 Hatimaye Yoshua na Waisraeli wote wakarudi kambini Gilgali.+
11 Mara tu Yabini mfalme wa Hasori aliposikia habari hizo, akatuma ujumbe kwa Yobabu mfalme wa Madoni,+ na kwa mfalme wa Shimroni, na mfalme wa Akshafi,+ 2 wafalme wa eneo la kaskazini lenye milima, wa maeneo tambarare* upande wa kusini wa Kinerethi, wale waliokuwa Shefela na kwenye miteremko ya Dori+ upande wa magharibi, 3 Wakanaani+ upande wa mashariki na magharibi, Waamori,+ Wahiti, Waperizi, Wayebusi katika eneo lenye milima, na Wahivi+ chini ya Mlima Hermoni+ katika nchi ya Mispa. 4 Basi wakatoka na majeshi yao yote, watu wengi sana kama chembe za mchanga kwenye ufuo wa bahari, pamoja na farasi na magari mengi sana ya vita. 5 Wafalme hao wote wakakubaliana kukutana, nao wakaja na kupiga kambi karibu na chemchemi ya Meromu ili kupigana na Waisraeli.
6 Ndipo Yehova akamwambia Yoshua: “Usiwaogope+ kwa sababu kesho, wakati kama huu, nitawatia wote mikononi mwa Waisraeli, nanyi mtawaangamiza. Mtakata mishipa ya miguu ya farasi wao,+ na kuyachoma moto magari yao.” 7 Basi Yoshua na wanajeshi wake wote wakawashambulia ghafla karibu na chemchemi ya Meromu. 8 Yehova akawatia mikononi mwa Waisraeli,+ nao wakawashinda na kuwakimbiza mpaka Sidoni Kuu+ na Misrefoth-maimu+ na Bonde la Mispe upande wa mashariki, nao wakawaangamiza, na hakuna yeyote aliyebaki.+ 9 Kisha Yoshua akawatendea kama Yehova alivyokuwa amemwambia; akakata mishipa ya miguu ya farasi wao na kuchoma moto magari yao.+
10 Yoshua akarudi na kuliteka Hasori, akamuua mfalme wake kwa upanga,+ kwa sababu Hasori lilikuwa jiji kuu kati ya falme hizo zote. 11 Wakawaangamiza wakaaji wote* kwa upanga.+ Hakuna kiumbe yeyote anayepumua aliyebaki.+ Kisha akaliteketeza Hasori. 12 Yoshua akayateka majiji yote ya wafalme hao na kuwashinda wafalme wote kwa upanga.+ Akawaangamiza,+ kama Musa mtumishi wa Yehova alivyoamuru. 13 Hata hivyo, Waisraeli hawakuteketeza jiji lolote lililokuwa vilimani isipokuwa Hasori ambalo liliteketezwa na Yoshua. 14 Waisraeli wakajichukulia nyara zote na mifugo katika majiji hayo.+ Lakini wakawaangamiza wanadamu wote kwa upanga.+ Hawakumwacha mtu yeyote anayepumua.+ 15 Kama Yehova alivyomwamuru Musa mtumishi wake, ndivyo Musa alivyomwamuru Yoshua,+ na ndivyo Yoshua alivyofanya. Hakuna jambo lolote ambalo hakufanya kati ya mambo yote ambayo Yehova alimwamuru Musa.+
16 Yoshua aliiteka nchi hii yote: eneo lenye milima, eneo lote la Negebu,+ nchi yote ya Gosheni, Shefela,+ Araba,+ na eneo lenye milima la Israeli na maeneo yake ya Shefela,* 17 kuanzia Mlima Halaki, unaopanda hadi Seiri, na hadi Baal-gadi+ katika Bonde la Lebanoni chini ya Mlima Hermoni,+ naye akawashinda, akawakamata, na kuwaua wafalme wote wa maeneo hayo. 18 Yoshua alipigana na wafalme hao wote kwa muda mrefu. 19 Hakuna jiji lolote lililofanya amani na Waisraeli isipokuwa Wahivi waliokaa Gibeoni.+ Waisraeli walipigana na majiji mengine yote na kuyashinda.+ 20 Yehova aliacha mioyo yao iwe mikaidi+ hivi kwamba wakapigana na Waisraeli, ili awaangamize bila huruma.+ Walipaswa kuangamizwa, kama Yehova alivyomwamuru Musa.+
21 Wakati huo, Yoshua aliwaangamiza kabisa Waanaki+ kutoka katika eneo lenye milima, Hebroni, Debiri, Anabu, na kutoka katika eneo lote lenye milima la Yuda na Israeli. Yoshua aliwaangamiza watu hao na majiji yao.+ 22 Waanaki hawakubaki katika nchi ya Waisraeli; walibaki+ tu Gaza,+ Gathi,+ na Ashdodi.+ 23 Basi Yoshua akachukua nchi yote, kama Yehova alivyomwahidi Musa,+ Yoshua akawapa Waisraeli iwe urithi wao ili igawanywe kulingana na makabila yao.+ Nchi ikawa na amani bila vita.+
12 Basi hawa ndio wafalme ambao Waisraeli waliwashinda na kumiliki nchi yao upande wa mashariki wa Yordani, kuanzia Bonde* la Arnoni+ hadi Mlima Hermoni+ na eneo lote la Araba kuelekea upande wa mashariki:+ 2 Mfalme Sihoni+ wa Waamori, aliyeishi Heshboni na kutawala kutoka Aroeri,+ kwenye ukingo wa Bonde* la Arnoni,+ na kutoka katikati ya bonde hilo, na nusu ya Gileadi hadi Bonde la Yaboki, kwenye mpaka wa Waamoni. 3 Alitawala pia Araba hadi Bahari ya Kinerethi*+ kuelekea mashariki hadi Bahari ya Araba, yaani, Bahari ya Chumvi, upande wa mashariki kuelekea Beth-yeshimothi, na kuelekea kusini chini ya miteremko ya Pisga.+
4 Pia, eneo la Mfalme Ogu+ wa Bashani, aliyekuwa kati ya Warefaimu+ waliosalia, ambaye aliishi Ashtarothi na Edrei 5 na kutawala katika eneo la Mlima Hermoni, Saleka, na Bashani yote,+ hadi mpaka wa Wageshuri na Wamaakathi,+ na nusu ya Gileadi, hadi katika eneo la Mfalme Sihoni wa Heshboni.+
6 Musa mtumishi wa Yehova pamoja na Waisraeli waliwashinda,+ kisha Musa mtumishi wa Yehova akawapa nchi hiyo watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase ili waimiliki.+
7 Hawa ndio wafalme ambao Yoshua na Waisraeli waliwashinda upande wa magharibi wa Yordani, kuanzia Baal-gadi+ katika Bonde la Lebanoni+ hadi Mlima Halaki,+ unaopanda hadi Seiri,+ halafu Yoshua akayapa makabila ya Israeli nchi yao ili waimiliki na kugawana kulingana na makabila yao,+ 8 katika eneo lenye milima, Shefela, Araba, kwenye miteremko, nyikani, na katika Negebu+—nchi ya Wahiti, Waamori,+ Wakanaani, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi:+
9 Mfalme wa Yeriko,+ mfalme wa Ai,+ jiji lililokuwa kando ya Betheli,
10 mfalme wa Yerusalemu, mfalme wa Hebroni,+
11 mfalme wa Yarmuthi, mfalme wa Lakishi,
12 mfalme wa Egloni, mfalme wa Gezeri,+
13 mfalme wa Debiri,+ mfalme wa Gederi,
14 mfalme wa Horma, mfalme wa Aradi,
15 mfalme wa Libna,+ mfalme wa Adulamu,
16 mfalme wa Makeda,+ mfalme wa Betheli,+
17 mfalme wa Tapua, mfalme wa Heferi,
18 mfalme wa Afeki, mfalme wa Lasharoni,
19 mfalme wa Madoni, mfalme wa Hasori,+
20 mfalme wa Shimron-meroni, mfalme wa Akshafi,
21 mfalme wa Taanaki, mfalme wa Megido,
22 mfalme wa Kedeshi, mfalme wa Yokneamu+ kule Karmeli,
23 mfalme wa Dori kwenye miteremko ya Dori,+ mfalme wa Goiimu kule Gilgali,
24 na mfalme wa Tirsa; jumla ya wafalme hao ni 31.
13 Basi Yoshua alikuwa amezeeka na umri wake ulikuwa umesonga sana.+ Kwa hiyo Yehova akamwambia, “Umezeeka na umri wako umesonga sana; na bado hamjamiliki* sehemu kubwa ya nchi. 2 Hii ndiyo nchi ambayo imebaki:+ maeneo yote ya Wafilisti na ya Wageshuri+ 3 (kuanzia kijito cha Mto Nile* kilicho upande wa mashariki wa* Misri hadi kwenye mpaka wa Ekroni upande wa kaskazini, eneo lililoonwa kuwa sehemu ya Wakanaani)+ kutia ndani eneo la watawala watano wa Wafilisti+—Wagaza, Waashdodi,+ Waashkeloni,+ Wagathi,+ Waekroni;+ eneo la Waavimu+ 4 upande wa kusini; nchi yote ya Wakanaani; Meara, ambayo ni ya Wasidoni,+ hadi Afeki, kwenye mpaka wa Waamori; 5 nchi ya Wagebali+ na nchi yote ya Lebanoni kuelekea mashariki, kuanzia Baal-gadi chini ya Mlima Hermoni hadi Lebo-hamathi;*+ 6 wakaaji wote wa eneo lenye milima kuanzia Lebanoni+ hadi Misrefoth-maimu;+ na Wasidoni wote.+ Nitawafukuza* mbele ya Waisraeli.+ Utaigawanya nchi hiyo na kuwapa Waisraeli kuwa urithi wao, kama nilivyokuamuru.+ 7 Na sasa yagawie makabila tisa pamoja na nusu ya kabila la Manase nchi hii kuwa urithi wao.”+
8 Nusu iliyobaki ya kabila la Manase, pamoja na watu wa kabila la Rubeni na Gadi walichukua urithi wao waliopewa na Musa upande wa mashariki wa Yordani, kama tu Musa mtumishi wa Yehova alivyowapa:+ 9 kuanzia Aroeri,+ kwenye ukingo wa Bonde* la Arnoni,+ na jiji lililo katikati ya bonde hilo, na uwanda wote wa juu wa Medeba hadi Diboni; 10 na majiji yote ya Mfalme Sihoni wa Waamori, aliyetawala Heshboni, hadi kwenye mpaka wa Waamoni;+ 11 pia Gileadi na eneo la Wageshuri na Wamaakathi+ na eneo lote la Mlima Hermoni na Bashani+ hadi Saleka;+ 12 ufalme wote wa Ogu kule Bashani, aliyetawala Ashtarothi na Edrei. (Alikuwa kati ya Warefaimu waliobaki.)+ Musa aliwashinda na kuwafukuza.*+ 13 Lakini Waisraeli hawakuwafukuza*+ Wageshuri na Wamaakathi, kwa kuwa Wageshuri na Wamaakathi wanaishi miongoni mwa Waisraeli mpaka leo.
14 Musa hakuwapa watu wa kabila la Lawi urithi.+ Urithi wao ni dhabihu zinazochomwa kwa moto zinazotolewa kwa Yehova Mungu wa Israeli,+ kama alivyowaahidi.+
15 Ndipo Musa akawapa urithi watu wa kabila la Rubeni kulingana na koo zao, 16 na eneo lao lilianzia Aroeri, kwenye ukingo wa Bonde* la Arnoni, na jiji lililo katikati ya bonde hilo, na uwanda wote wa juu wa Medeba; 17 Heshboni na miji yake yote+ iliyo kwenye uwanda wa juu, Diboni, Bamoth-baali, Beth-baal-meoni,+ 18 Yahazi,+ Kedemothi,+ Mefaathi,+ 19 Kiriathaimu, Sibma,+ na Sereth-shahari kwenye mlima wa bondeni,* 20 Beth-peori, miteremko ya Pisga,+ Beth-yeshimothi,+ 21 majiji yote kwenye uwanda wa juu, na eneo lote la Mfalme Sihoni wa Waamori, aliyetawala Heshboni.+ Musa alimshinda yeye+ pamoja na wakuu wa Midiani, yaani, Evi, Rekemu, Suri, Huru, na Reba,+ watawala vibaraka* wa Sihoni waliokaa nchini humo. 22 Waisraeli walimuua kwa upanga Balaamu+ mwana wa Beori, yule mbashiri,*+ pamoja na watu wengine. 23 Na mpaka wa kabila la Rubeni ulikuwa Yordani; na eneo hilo lilikuwa urithi wa kabila la Rubeni kulingana na koo zao, pamoja na miji na vijiji vyake.
24 Pia, Musa akawapa urithi watu wa kabila la Gadi, kulingana na koo zao, 25 na eneo lao lilitia ndani Yazeri+ na majiji yote ya Gileadi na nusu ya nchi ya Waamoni+ hadi Aroeri, mbele ya Raba;+ 26 na kutoka Heshboni+ hadi Ramath-mispe na Betonimu, na kutoka Mahanaimu+ hadi mpaka wa Debiri; 27 na bondeni,* Beth-haramu, Beth-nimra,+ Sukothi,+ na Safoni, eneo lililobaki la Mfalme Sihoni wa Heshboni,+ na Mto Yordani ulikuwa mpaka ulioanzia upande wa chini wa Bahari ya Kinerethi,*+ upande wa mashariki wa Yordani. 28 Huo ndio uliokuwa urithi wa kabila la Gadi kulingana na koo zao, pamoja na miji na vijiji vyake.
29 Pia, Musa akawapa urithi nusu ya watu wa kabila la Manase, ukawa urithi wao kulingana na koo zao.+ 30 Na eneo lao lilianzia Mahanaimu+ na eneo lote la Bashani, eneo lote la Mfalme Ogu wa Bashani, na vijiji vyote vya mahema vya Yairi+ kule Bashani, miji 60. 31 Na nusu ya eneo la Gileadi, na Ashtarothi na Edrei,+ majiji ya ufalme wa Ogu kule Bashani, yalichukuliwa na wana wa Makiri+ mwana wa Manase, yaani, nusu ya wana wa Makiri kulingana na koo zao.
32 Huo ndio urithi ambao Musa aliwapa katika maeneo tambarare ya jangwani ya Moabu ng’ambo ya Yordani, upande wa mashariki wa Yeriko.+
33 Lakini Musa hakuwapa urithi watu wa kabila la Lawi.+ Yehova Mungu wa Israeli ndiye urithi wao, kama alivyowaahidi.+
14 Basi huu ndio urithi ambao kuhani Eleazari, Yoshua mwana wa Nuni, na viongozi wa koo* za makabila ya Israeli waliwapa Waisraeli katika nchi ya Kanaani.+ 2 Waligawiwa urithi wao kwa kura,+ kama Yehova alivyomwagiza Musa ayagawie yale makabila tisa na nusu.+ 3 Musa alikuwa tayari ameyapa makabila mawili na nusu urithi ng’ambo ya* Yordani,+ lakini hakuwapa Walawi urithi kati yao.+ 4 Wazao wa Yosefu walihesabiwa kuwa makabila mawili,+ Manase na Efraimu;+ nao hawakuwagawia Walawi urithi nchini, isipokuwa majiji+ ya kuishi na malisho kwa ajili ya mifugo yao na mali zao.+ 5 Basi, Waisraeli waliigawanya nchi kama Yehova alivyomwamuru Musa.
6 Ndipo watu wa kabila la Yuda wakaenda kwa Yoshua kule Gilgali,+ na Kalebu+ mwana wa Yefune Mkenizi akamwambia: “Unajua vizuri maneno ambayo Yehova alimwambia Musa+ mtumishi wa Mungu wa kweli+ juu yangu na juu yako kule Kadesh-barnea.+ 7 Nilikuwa na umri wa miaka 40 Musa mtumishi wa Yehova aliponituma kutoka Kadesh-barnea kwenda kuipeleleza nchi,+ nami nikamletea habari ya kweli.*+ 8 Ingawa ndugu zangu walioenda pamoja nami waliwavunja watu moyo,* mimi nilimfuata Yehova Mungu wangu kwa moyo wote.*+ 9 Siku hiyo, Musa aliapa hivi: ‘Nchi ambayo mguu wako umekanyaga itakuwa urithi wako na wa wana wako milele, kwa sababu umemfuata Yehova Mungu wangu kwa moyo wote.’+ 10 Basi kama alivyoahidi,+ Yehova amenihifadhi hai+ kwa miaka 45 tangu Yehova alipompa Musa ahadi hiyo Waisraeli walipotembea nyikani;+ ningali hai leo, nina umri wa miaka 85. 11 Lakini bado nina nguvu nilizokuwa nazo siku ambayo Musa alinituma. Bado nina nguvu nilizokuwa nazo wakati huo za kupigana vitani na kufanya kazi nyingine. 12 Kwa hiyo, nipe eneo hili lenye milima ambalo Yehova aliahidi siku hiyo. Ingawa ulisikia siku hiyo kwamba kuna Waanaki+ wanaoishi huko katika majiji makubwa yenye ngome,+ bila shaka* Yehova atakuwa pamoja nami,+ nami nitawafukuza,* kama Yehova alivyoahidi.”+
13 Ndipo Yoshua akambariki Kalebu mwana wa Yefune na kumpa Hebroni kuwa urithi wake.+ 14 Ndiyo sababu Hebroni limekuwa urithi wa Kalebu mwana wa Yefune Mkenizi mpaka leo, kwa sababu alimfuata Yehova Mungu wa Israeli kwa moyo wote.+ 15 Hapo awali Hebroni liliitwa Kiriath-arba+ (Arba alikuwa mtu maarufu miongoni mwa Waanaki). Nchi ikawa na amani bila vita.+
15 Nchi ambayo watu wa kabila la Yuda waligawiwa*+ kwa ajili ya koo zao ilifika kwenye mpaka wa Edomu,+ nyika ya Zini, hadi upande wa kusini kabisa wa Negebu. 2 Mpaka wao wa kusini ulianzia mwisho wa Bahari ya Chumvi,+ yaani, kuanzia mahali ambapo mto unaingia baharini upande wa kusini. 3 Na uliendelea upande wa kusini kwenye mwinuko wa Akrabimu,+ ukavuka hadi Zini, na kupanda kutoka kusini hadi Kadesh-barnea,+ kufika Hezroni, Adari, na kuzunguka hadi Karka. 4 Kisha ukaendelea hadi Asimoni+ na kufika kwenye Korongo la Misri,+ nao ukafikia mwisho kwenye Bahari.* Huo ndio uliokuwa mpaka wao wa kusini.
5 Mpaka wa mashariki ulianzia kwenye Bahari ya Chumvi hadi mahali ambapo Mto Yordani unaingia katika Bahari ya Chumvi, na mpaka wa kaskazini ulianzia mahali ambapo Mto Yordani unaingia katika Bahari ya Chumvi.+ 6 Mpaka huo ulipanda hadi Beth-hogla+ na kuvuka upande wa kaskazini wa Beth-araba,+ nao uliendelea juu mpaka kwenye jiwe la Bohani+ mwana wa Rubeni. 7 Na mpaka huo ukapanda hadi Debiri katika Bonde la* Akori+ na kugeuka kuelekea kaskazini hadi Gilgali,+ mbele ya njia inayopanda kuelekea Adumimu, ambayo iko upande wa kusini wa bonde la mto, kisha ukaendelea hadi kwenye chemchemi ya En-shemeshi+ na kufikia mwisho kule En-rogeli.+ 8 Na mpaka huo ukapanda hadi Bonde la Mwana wa Hinomu+ kwenye mteremko wa jiji la Wayebusi+ upande wa kusini, yaani, Yerusalemu,+ nao ukapanda hadi juu ya mlima unaotazamana na Bonde la Hinomu upande wa magharibi, yaani, mwisho kabisa wa Bonde la* Refaimu upande wa kaskazini. 9 Mpaka huo ulianzia juu ya mlima hadi chemchemi ya Neftoa+ mpaka kwenye majiji ya Mlima Efroni; nao ulifika Baala, yaani, Kiriath-yearimu.+ 10 Kisha ukazunguka kutoka Baala kuelekea upande wa magharibi hadi Mlima Seiri, ukaendelea hadi kwenye mteremko wa Mlima Yearimu upande wa kaskazini, yaani, Kesaloni, nao ukashuka hadi Beth-shemeshi+ na kuendelea hadi Timna.+ 11 Kisha ukaendelea hadi kwenye mteremko wa kaskazini wa Ekroni,+ hadi Shikeroni, kufika kwenye Mlima Baala na kuendelea hadi Yabneeli, nao ulifikia mwisho kwenye bahari.
12 Mpaka wa magharibi ulikuwa Bahari Kuu*+ na pwani yake. Hiyo ndiyo iliyokuwa mipaka yote ya wazao wa Yuda kulingana na koo zao.
13 Naye Yoshua akampa Kalebu+ mwana wa Yefune sehemu ya nchi kati ya wazao wa Yuda kama Yehova alivyomwagiza Yoshua, yaani, eneo la Kiriath-arba (Arba alikuwa baba ya Waanaki), yaani, Hebroni.+ 14 Basi Kalebu aliwafukuza kutoka Hebroni wana watatu wa Anaki:+ Sheshai, Ahimani, Talmai,+ yaani, wazao wa Anaki. 15 Kisha akapanda kutoka huko na kwenda kuwashambulia wakaaji wa Debiri.+ (Hapo awali Debiri liliitwa Kiriath-seferi.) 16 Ndipo Kalebu akasema: “Yeyote atakayeshambulia na kuteka jiji la Kiriath-seferi, nitampa binti yangu Aksa awe mke wake.” 17 Othnieli+ mwana wa Kenasi,+ ndugu ya Kalebu, akaliteka. Kwa hiyo akampa Aksa+ binti yake awe mke wake. 18 Mwanamke huyo alipokuwa akienda nyumbani kwake, akamsihi mume wake amwombe baba* yake shamba. Kisha mwanamke huyo akashuka kutoka juu ya punda wake.* Kalebu akamuuliza: “Unataka nini?”+ 19 Akamwambia: “Tafadhali nibariki, kwa maana umenipa shamba upande wa kusini;* nipe pia Guloth-maimu.”* Basi Kalebu akampa Gulothi ya Juu na Gulothi ya Chini.
20 Huo ndio uliokuwa urithi wa watu wa kabila la Yuda kulingana na koo zao.
21 Na majiji yaliyokuwa upande wa kusini kabisa wa kabila la Yuda kuelekea mpaka wa Edomu+ yalikuwa Kabzeeli, Ederi, Yaguri, 22 Kina, Dimona, Adada, 23 Kedeshi, Hasori, Ithnani, 24 Zifu, Telemu, Bealothi, 25 Hasor-hadata, na Kerioth-hesroni, yaani, Hasori, 26 Amamu, Shema, Molada,+ 27 Hasar-gada, Heshmoni, Beth-peleti,+ 28 Hasar-shuali, Beer-sheba,+ Biziothia, 29 Baala, Iimu, Esemu, 30 Eltoladi, Kesili, Horma,+ 31 Siklagi,+ Madmana, Sansana, 32 Lebaothi, Shilhimu, Aini, na Rimoni+—jumla ya majiji 29, pamoja na vijiji vyake.
33 Majiji yaliyokuwa Shefela+ yalikuwa Eshtaoli, Sora,+ Ashna, 34 Zanoa, En-ganimu, Tapua, Enamu, 35 Yarmuthi, Adulamu,+ Soko, Azeka,+ 36 Shaaraimu,+ Adithaimu, na Gedera, na Gederothaimu*—majiji 14 na vijiji vyake.
37 Senani, Hadasha, Migdal-gadi, 38 Dileani, Mispe, Yoktheeli, 39 Lakishi,+ Boskathi, Egloni, 40 Kaboni, Lahmamu, Kitilishi, 41 Gederothi, Beth-dagoni, Naama, na Makeda+—majiji 16 na vijiji vyake.
42 Libna,+ Etheri, Ashani,+ 43 Ifta, Ashna, Nesibu, 44 Keila, Akzibu, na Maresha—majiji tisa na vijiji vyake.
45 Ekroni na miji na vijiji vyake; 46 kuanzia Ekroni kuelekea magharibi, miji yote iliyo kando ya Ashdodi na vijiji vyake.
47 Ashdodi,+ miji na vijiji vyake; Gaza,+ miji na vijiji vyake, hadi kwenye Bonde la Misri, na Bahari Kuu,* na eneo jirani.+
48 Na katika eneo lenye milima, Shamiri, Yatiri,+ Soko, 49 Dana, Kiriath-sana, yaani, Debiri, 50 Anabu, Eshtemo,+ Animu, 51 Gosheni,+ Holoni, na Gilo+—majiji 11 na vijiji vyake.
52 Arabu, Duma, Eshani, 53 Yanimu, Beth-tapua, Afeka, 54 Humta, Kiriath-arba, yaani, Hebroni,+ na Siori—majiji tisa na vijiji vyake.
55 Maoni,+ Karmeli, Zifu,+ Yuta, 56 Yezreeli, Yokdeamu, Zanoa, 57 Kayini, Gibea, Timna+—majiji kumi na vijiji vyake.
58 Halhuli, Beth-suri, Gedori, 59 Maarathi, Beth-anothi, na Eltekoni—majiji sita na vijiji vyake.
60 Kiriath-baali, yaani, Kiriath-yearimu,+ na Raba—majiji mawili na vijiji vyake.
61 Katika nyika, Beth-araba,+ Midini, Sekaka, 62 Nibshani, Jiji la Chumvi, na En-gedi+—majiji sita na vijiji vyake.
63 Lakini watu wa kabila la Yuda hawakuwafukuza+ Wayebusi+ waliokuwa wakikaa Yerusalemu,+ basi tangu wakati huo Wayebusi wanakaa Yerusalemu pamoja na watu wa kabila la Yuda.
16 Na nchi ambayo wazao wa Yosefu+ waligawiwa*+ ilianzia Yordani huko Yeriko hadi kwenye vijito vilivyo upande wa mashariki wa Yeriko, na kupitia nyikani hadi Yeriko katika eneo lenye milima la Betheli.+ 2 Ilianzia Betheli ambayo ni sehemu ya Luzi na kuendelea hadi kwenye mpaka wa Waarki huko Atarothi, 3 nayo ikashuka kwenda magharibi hadi kwenye mpaka wa Wayafleti kufikia mpaka wa Beth-horoni+ ya Chini na Gezeri,+ na kufika kwenye bahari.
4 Na wazao wa Yosefu,+ yaani, watu wa kabila la Manase na kabila la Efraimu, wakamiliki nchi yao.+ 5 Na huu ndio mpaka wa wazao wa Efraimu kulingana na koo zao: Mpaka wa urithi wao upande wa mashariki ulikuwa Ataroth-adari,+ hadi Beth-horoni ya Juu,+ 6 na mpaka huo ulifika kwenye bahari. Mikmethathi+ ilikuwa upande wa kaskazini, na mpaka huo ulizunguka upande wa mashariki hadi Taanath-shilo, kuelekea upande wa mashariki hadi Yanoa. 7 Kisha ukashuka kutoka Yanoa hadi Atarothi na Naara na kupita Yeriko+ hadi Yordani. 8 Kutoka Tapua+ ukaelekea magharibi hadi kwenye Bonde la Kana, na kufika kwenye bahari.+ Huo ndio urithi wa kabila la Efraimu kulingana na koo zao; 9 na wazao wa Efraimu walikuwa pia na majiji yaliyozungukwa katikati ya urithi wa wazao wa Manase.+
10 Lakini hawakuwafukuza Wakanaani waliokuwa wakikaa Gezeri,+ na tangu wakati huo Wakanaani wanaishi miongoni mwa wazao wa Efraimu+ wakifanya kazi za kulazimishwa.+
17 Kisha watu wa kabila la Manase,+ mzaliwa wa kwanza wa Yosefu,+ wakagawiwa nchi yao kwa kura.+ Makiri,+ mzaliwa wa kwanza wa Manase na baba ya Gileadi, alikuwa amepewa nchi ya Gileadi na Bashani+ kwa sababu alikuwa mwanajeshi hodari. 2 Wazao waliobaki wa Manase waligawiwa nchi yao kwa kura kulingana na koo zao, yaani, wana wa Abiezeri,+ wana wa Heleki, wana wa Asrieli, wana wa Shekemu, wana wa Heferi, na wana wa Shemida. Hao ndio wazao wa kiume wa Manase mwana wa Yosefu, kulingana na koo zao.+ 3 Lakini Selofehadi+ mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, hakuwa na watoto wa kiume ila mabinti, na majina ya mabinti hao yalikuwa: Mala, Noa, Hogla, Milka, na Tirsa. 4 Basi wakaja kwa kuhani Eleazari,+ Yoshua mwana wa Nuni, na wakuu na kuwaambia: “Yehova ndiye aliyemwamuru Musa atupe urithi miongoni mwa ndugu zetu.”+ Basi akawapa urithi kati ya ndugu za baba yao kwa agizo la Yehova.+
5 Na watu wa kabila la Manase walipewa pia maeneo mengine kumi zaidi ya nchi ya Gileadi na Bashani, ng’ambo ya* Yordani,+ 6 kwa kuwa binti za Manase walipokea pia urithi pamoja na wanawe, na nchi ya Gileadi ikawa mali ya wazao waliobaki wa Manase.
7 Na mpaka wa Manase ulianzia Asheri hadi Mikmethathi,+ mbele ya Shekemu,+ na kuendelea hadi upande wa kusini* wa nchi ya wakaaji wa En-Tapua. 8 Nchi ya Tapua+ ikawa ya Manase lakini mji wa Tapua uliokuwa kwenye mpaka wa nchi ya Manase ulikuwa wa wazao wa Efraimu. 9 Na mpaka huo ulishuka hadi kwenye Bonde la Kana, upande wa kusini. Watu wa kabila la Efraimu walikuwa na majiji miongoni mwa majiji ya kabila la Manase,+ na mpaka wa Manase ulikuwa upande wa kaskazini wa bonde la mto, nao ulifika kwenye bahari.+ 10 Upande wa kusini ulikuwa wa kabila la Efraimu, na upande wa kaskazini ulikuwa wa Manase, na mpaka wake ulikuwa bahari,+ na mpaka wa kaskazini* ulifika kwenye eneo la Asheri na mpaka wa mashariki ulifika kwenye eneo la Isakari.
11 Katika maeneo ya Isakari na Asheri, watu wa kabila la Manase walipewa Beth-sheani na miji yake, Ibleamu+ na miji yake, Dori+ na miji yake, En-dori+ na miji yake, Taanaki+ na miji yake, Megido na miji yake, maeneo matatu yenye milima.
12 Lakini wazao wa Manase hawakumiliki majiji hayo; Wakanaani waliendelea kukaa katika nchi hiyo.+ 13 Waisraeli walipopata nguvu, waliwatumikisha Wakanaani,+ lakini hawakuwafukuza* wote.+
14 Wazao wa Yosefu wakamuuliza Yoshua: “Kwa nini umetupatia eneo moja tu kwa kura+ na sehemu moja kuwa urithi wetu? Tuko wengi sana kwa sababu Yehova ametubariki mpaka sasa.”+ 15 Yoshua akawajibu: “Ikiwa ninyi ni wengi sana na eneo lenye milima la Efraimu+ haliwatoshi, pandeni msituni katika nchi ya Waperizi+ na Warefaimu,+ mkaufyeke msitu ili mpate makao huko.” 16 Kisha wazao wa Yosefu wakasema: “Eneo lenye milima halitutoshi, na Wakanaani wote wanaokaa bondeni,* yaani, wale wanaokaa Beth-sheani+ na miji yake na wale wanaokaa katika Bonde la* Yezreeli,+ wana magari ya vita+ yenye miundu ya chuma.”* 17 Basi Yoshua akaiambia hivi nyumba ya Yosefu, yaani, kabila la Efraimu na Manase: “Ninyi ni wengi sana, nanyi mna nguvu nyingi. Hamtapata eneo moja tu,+ 18 eneo lenye milima litakuwa lenu pia.+ Ingawa ni msitu, ufyekeni, utakuwa mwisho wa eneo lenu. Mtawafukuza Wakanaani, hata kama wana nguvu na wana magari ya vita yenye miundu ya chuma.”*+
18 Baada ya kuitiisha nchi,+ Waisraeli wote wakakusanyika Shilo+ na kupiga hema la mkutano+ huko. 2 Lakini makabila saba ya Waisraeli bado hayakuwa yamegawiwa urithi wao. 3 Ndipo Yoshua akawaambia Waisraeli: “Mtakawia mpaka lini kumiliki nchi ambayo Yehova Mungu wa mababu zenu amewapa?+ 4 Chagueni wanaume watatu kutoka kila kabila ili niwatume; watazunguka katika nchi yote na kuchora ramani kulingana na urithi wao. Kisha wataniletea habari. 5 Wataigawanya nchi hiyo katika maeneo saba.+ Kabila la Yuda litabaki katika eneo lake upande wa kusini,+ na nyumba ya Yosefu itabaki katika eneo lake upande wa kaskazini.+ 6 Igawanyeni nchi katika maeneo saba na kuniletea ramani yake, nami nitawapa urithi kwa kupiga kura+ mbele za Yehova Mungu wetu. 7 Lakini Walawi hawana urithi kati yenu,+ kwa sababu ukuhani wa Yehova ndio urithi wao;+ na tayari Gadi, Rubeni, na nusu ya kabila la Manase+ wamechukua urithi wao upande wa mashariki wa Yordani, ambao Musa mtumishi wa Yehova aliwapa.”
8 Wanaume hao wakajitayarisha kwenda kuchora ramani ya nchi, naye Yoshua akawaambia hivi: “Nendeni mkazunguke katika nchi yote, mchore ramani yake na kuniletea habari, nami nitawapa urithi kwa kupiga kura mbele za Yehova hapa Shilo.”+ 9 Basi wanaume hao wakaenda, wakazunguka nchini na kuchora ramani yenye maeneo saba kulingana na majiji, wakaandika habari hizo katika kitabu. Kisha wakarudi kwa Yoshua kambini huko Shilo. 10 Ndipo Yoshua akapiga kura kwa ajili ya maeneo hayo mbele za Yehova.+ Kisha Yoshua akawagawia Waisraeli nchi kulingana na makabila yao.+
11 Kabila la Benjamini liligawiwa urithi wao kwa kura kulingana na koo zao, walipewa urithi kati ya kabila la Yuda+ na wazao wa Yosefu.+ 12 Mpaka wao wa kaskazini ulianzia Yordani, na kwenda kaskazini kwenye mteremko wa Yeriko+ na kupanda mlimani upande wa magharibi, hadi katika nyika ya Beth-aveni.+ 13 Kisha ukaendelea mpaka Luzi kwenye mteremko wa kusini wa Luzi, yaani, Betheli;+ nao ukashuka hadi Ataroth-adari+ kwenye mlima ulio upande wa kusini wa Beth-horoni ya Chini.+ 14 Na mpaka huo uligeuka upande wa magharibi kuelekea kusini kutoka kwenye mlima unaotazamana na Beth-horoni upande wa kusini; nao ukafika Kiriath-baali, yaani, Kiriath-yearimu,+ jiji la Yuda. Huo ndio mpaka wa magharibi.
15 Mpaka wa kusini ulianzia mwisho wa jiji la Kiriath-yearimu, na kuelekea upande wa magharibi; kisha ukafika kwenye chemchemi ya Neftoa.+ 16 Nao ulishuka hadi mwisho wa mlima unaotazamana na Bonde la Mwana wa Hinomu,+ upande wa kaskazini katika Bonde* la Refaimu,+ nao ukashuka upande wa kusini katika Bonde la Hinomu, kwenye mteremko wa Myebusi,+ na kufika En-rogeli.+ 17 Kisha ulielekea kaskazini hadi En-shemeshi na kufika Gelilothi, mbele ya njia inayopanda kuelekea Adumimu,+ na kushuka kwenye jiwe+ la Bohani+ mwana wa Rubeni. 18 Ukaendelea hadi kwenye mteremko wa kaskazini mbele ya Araba na kushuka hadi Araba. 19 Kisha ukaendelea hadi kwenye mteremko wa kaskazini wa Beth-hogla,+ na kufika katika ghuba ya kaskazini ya Bahari ya Chumvi+ upande wa kusini wa Yordani. Huo ndio uliokuwa mpaka wa kusini. 20 Na Mto Yordani ulikuwa mpaka wa mashariki. Huo ndio uliokuwa urithi wa wazao wa Benjamini kulingana na koo zao, na hiyo ndiyo mipaka yao yote.
21 Na majiji ya kabila la Benjamini kulingana na koo zao yalikuwa: Yeriko, Beth-hogla, Emek-kesisi, 22 Beth-araba,+ Semaraimu, Betheli,+ 23 Avimu, Para, Ofra, 24 Kefar-amoni, Ofni, na Geba+—majiji 12 na vijiji vyake.
25 Gibeoni,+ Rama, Beerothi, 26 Mispe, Kefira, Mosa, 27 Rekemu, Irpeeli, Tarala, 28 Zela,+ Ha-elefu, Yebusi, yaani, Yerusalemu,+ Gibea,+ na Kiriathi—majiji 14 na vijiji vyake.
Huo ndio uliokuwa urithi wa wazao wa Benjamini kulingana na koo zao.
19 Kura ya pili+ ilikuwa ya Simeoni, kwa ajili ya kabila la Simeoni+ kulingana na koo zao. Nao walipewa urithi kati ya urithi wa kabila la Yuda.+ 2 Urithi wao ulikuwa Beer-sheba,+ Sheba, Molada,+ 3 Hasar-shuali,+ Bala, Esemu,+ 4 Eltoladi,+ Bethuli, Horma, 5 Siklagi,+ Beth-markabothi, Hasar-susa, 6 Beth-lebaothi,+ na Sharuheni—majiji 13 na vijiji vyake; 7 Aini, Rimoni, Etheri, na Ashani+—majiji manne na vijiji vyake; 8 na vijiji vyote vilivyozunguka majiji hayo mpaka Baalath-beeri, Rama ya kusini. Huo ndio uliokuwa urithi wa kabila la Simeoni kulingana na koo zao. 9 Kabila la Yuda lilikuwa na eneo kubwa sana, basi wazao wa Simeoni waligawiwa sehemu ya eneo hilo. Hivyo wazao wa Simeoni walipata urithi katikati ya kabila la Yuda.+
10 Kura ya tatu+ ilikuwa ya wazao wa Zabuloni+ kulingana na koo zao, na mpaka wa urithi wao ulifika Saridi. 11 Mpaka wao ulipanda upande wa magharibi kuelekea Mareali kufika Dabeshethi na kuingia bondeni* mbele ya Yokneamu. 12 Na kutoka Saridi, ulielekea upande wa mashariki, na kufika kwenye mpaka wa Kisloth-tabori na kuendelea hadi Daberathi+ na kupanda hadi Yafia. 13 Kisha ukaelekea mashariki hadi Gath-heferi+ na kufika Eth-kazini, hadi Rimoni, na kufika Nea. 14 Na mpaka huo uligeuka kuelekea Hanathoni upande wa kaskazini, na kufika kwenye Bonde la Iftah-eli, 15 na Katathi, Nahalali, Shimroni,+ Idala, na Bethlehemu+—majiji 12 na vijiji vyake. 16 Huo ndio uliokuwa urithi wa wazao wa Zabuloni kulingana na koo zao.+ Hayo ndiyo yaliyokuwa majiji na vijiji vyake.
17 Kura ya nne+ ilikuwa ya Isakari,+ kwa ajili ya wazao wa Isakari kulingana na koo zao. 18 Na mpaka wao ulifika Yezreeli,+ Kesulothi, Shunemu,+ 19 Hafaraimu, Shioni, Anaharathi, 20 Rabithi, Kishioni, Ebesi, 21 Remethi, En-ganimu,+ En-hada, na Beth-pasesi. 22 Na mpaka huo ulifika Tabori+ na Shahasuma na Beth-shemeshi, na kufika kwenye Mto Yordani—majiji 16 na vijiji vyake. 23 Huo ndio uliokuwa urithi wa kabila la Isakari kulingana na koo zao,+ majiji na vijiji vyake.
24 Kura ya tano+ ilikuwa ya kabila la Asheri+ kulingana na koo zao. 25 Mpaka wao ulipita Helkathi,+ Hali, Beteni, Akshafi, 26 Alameleki, Amadi, na Mishali. Nao ulifika upande wa magharibi hadi Karmeli+ na kuelekea Shihor-libnathi, 27 nao uligeuka na kuelekea Beth-dagoni upande wa mashariki na kufika Zabuloni na Bonde la Iftah-eli upande wa kaskazini, hadi Beth-emeki na Neieli, kisha ukaelekea Kabuli upande wa kushoto, 28 na Ebroni, Rehobu, Hamoni, na Kana hadi Sidoni Kuu.+ 29 Na mpaka huo ukageuka kurudi Rama na kufika kwenye jiji la Tiro lenye ngome.+ Kisha ukageuka kurudi Hosa, na kufika kwenye bahari katika eneo la Akzibu, 30 Uma, Afeki,+ na Rehobu+—majiji 22 na vijiji vyake. 31 Huo ndio uliokuwa urithi wa kabila la Asheri kulingana na koo zao.+ Hayo ndiyo yaliyokuwa majiji na vijiji vyake.
32 Kura ya sita+ ilikuwa ya wazao wa Naftali, kwa ajili ya wazao wa Naftali kulingana na koo zao. 33 Mpaka wao ulianzia Helefu, kutoka kwenye mti mkubwa kule Saananimu,+ kuelekea Adami-nekebu na Yabneeli hadi Lakumu; na kufika kwenye Mto Yordani. 34 Na kutoka huko ukageuka na kuelekea magharibi hadi Aznoth-tabori na kwenda Hukkoki mpaka Zabuloni upande wa kusini na kupakana na Asheri upande wa magharibi na kuendelea hadi Yuda, na kufika kwenye Mto Yordani upande wa mashariki. 35 Na majiji yenye ngome yalikuwa Sidimu, Seri, Hamathi,+ Rakathi, Kinerethi, 36 Adama, Rama, Hasori,+ 37 Kedeshi,+ Edrei, En-hasori, 38 Yironi, Migdal-eli, Horemu, Beth-anathi, na Beth-shemeshi+—majiji 19 na vijiji vyake. 39 Huo ndio uliokuwa urithi wa kabila la Naftali kulingana na koo zao,+ majiji na vijiji vyake.
40 Kura ya saba+ ilikuwa ya kabila la Dani+ kulingana na koo zao. 41 Na mpaka wa urithi wao ulipita Sora,+ Eshtaoli, Ir-shemeshi, 42 Shaalabini,+ Aiyaloni,+ Ithla, 43 Eloni, Timna,+ Ekroni,+ 44 Elteke, Gibethoni,+ Baalathi, 45 Yehudi, Bene-beraki, Gath-rimoni,+ 46 Me-yarkoni, na Rakoni, mpaka ukiwa mbele ya Yopa.+ 47 Lakini eneo la kabila la Dani halikuwatosha kwa sababu lilikuwa dogo.+ Basi wakaenda kushambulia jiji la Leshemu,+ wakaliteka na kuwaangamiza wakaaji wake kwa upanga. Wakalimiliki na kukaa ndani yake, kisha wakabadili jina Leshemu kuwa Dani, jina la babu yao.+ 48 Huo ndio uliokuwa urithi wa kabila la Dani kulingana na koo zao. Hayo ndiyo yaliyokuwa majiji na vijiji vyake.
49 Basi wakamaliza kugawanya nchi ya urithi kulingana na maeneo yake. Kisha Waisraeli wakampa Yoshua mwana wa Nuni urithi kati yao. 50 Kwa agizo la Yehova walimpa jiji ambalo aliomba, yaani, Timnath-sera,+ katika eneo lenye milima la Efraimu, akalijenga upya na kukaa ndani yake.
51 Huo ndio urithi ambao kuhani Eleazari, Yoshua mwana wa Nuni, na viongozi wa koo* za makabila ya Waisraeli waligawanya+ kwa kura kule Shilo+ mbele za Yehova, kwenye mlango wa hema la mkutano.+ Basi wakamaliza kuigawanya nchi.
20 Kisha Yehova akamwambia Yoshua: 2 “Waambie Waisraeli, ‘Jichagulieni majiji ya makimbilio+ kama nilivyowaambia kupitia Musa, 3 ili mtu atakayemuua mwenzake* bila kukusudia au bila kujua akimbilie humo. Atakimbilia humo ili kumkwepa mtu anayetaka kulipiza kisasi cha damu.+ 4 Ni lazima akimbilie mojawapo ya majiji hayo+ na kusimama langoni,+ kisha atawaambia wazee wa jiji hilo kesi yake. Nao lazima wampokee jijini na kumpa makao, naye ataishi pamoja nao. 5 Na yule anayetaka kulipiza kisasi cha damu akimfuatia, wazee hawapaswi kumtia muuaji huyo mikononi mwake, kwa maana alimuua mwenzake bila kukusudia,* wala hakuwa akimchukia.+ 6 Ni lazima akae ndani ya jiji hilo mpaka kesi yake itakaposikilizwa mbele ya kusanyiko,+ naye atabaki humo mpaka kuhani mkuu+ anayehudumu wakati huo atakapokufa. Kisha muuaji huyo anaweza kurudi nyumbani kwake katika jiji alilokimbia.’”+
7 Basi wakatenga majiji haya kuwa matakatifu: Kedeshi+ kule Galilaya katika eneo lenye milima la Naftali, Shekemu+ katika eneo lenye milima la Efraimu, na Kiriath-arba,+ yaani, Hebroni, katika eneo lenye milima la Yuda. 8 Na katika eneo la Yordani, upande wa mashariki wa Yeriko, wakachagua jiji la Beseri+ lililo nyikani kwenye uwanda wa juu katika eneo la kabila la Rubeni, Ramothi+ kule Gileadi katika eneo la kabila la Gadi, na Golani+ kule Bashani katika eneo la kabila la Manase.+
9 Hayo ndiyo majiji yaliyochaguliwa kwa ajili ya Waisraeli wote na wageni walioishi kati yao, ili mtu yeyote atakayemuua mwenzake bila kukusudia akimbilie humo,+ ili asiuawe na mtu anayetaka kulipiza kisasi cha damu mpaka kesi yake isikilizwe mbele ya kusanyiko.+
21 Viongozi wa koo* za Walawi wakaenda kwa kuhani Eleazari+ na Yoshua mwana wa Nuni na viongozi wa koo* za makabila ya Israeli, 2 wakawaambia hivi huko Shilo+ katika nchi ya Kanaani: “Yehova aliamuru kupitia Musa tupewe majiji ya kuishi na malisho ya mifugo yetu.”+ 3 Basi kwa agizo la Yehova, Waisraeli wakawapa Walawi majiji hayo+ na malisho yake kutoka katika urithi wao wenyewe.+
4 Kura ya kwanza ilikuwa ya koo za Wakohathi,+ na Walawi waliokuwa wazao wa kuhani Haruni walipewa majiji 13 kwa kura katika maeneo ya kabila la Yuda,+ kabila la Simeoni,+ na kabila la Benjamini.+
5 Na Wakohathi waliobaki walipewa majiji kumi kwa kura katika maeneo ya koo za kabila la Efraimu,+ Dani, na katika eneo la nusu ya kabila la Manase.+
6 Na Wagershoni+ walipewa majiji 13 kwa kura katika maeneo ya koo za kabila la Isakari, Asheri, Naftali, na katika eneo la nusu ya kabila la Manase kule Bashani.+
7 Na Wamerari+ walipewa majiji 12 kulingana na koo zao katika maeneo ya kabila la Rubeni, Gadi, na Zabuloni.+
8 Hivyo Waisraeli wakawapa Walawi majiji hayo na malisho yake kwa kura kama Yehova alivyokuwa ameamuru kupitia Musa.+
9 Yafuatayo ni majina ya majiji+ katika maeneo ya kabila la Yuda na kabila la Simeoni ambayo waliwapa 10 wana wa Haruni wa koo za Walawi Wakohathi, kwa kuwa kura ya kwanza ilikuwa yao. 11 Waliwapa Kiriath-arba+ (Arba alikuwa baba ya Waanaki), yaani, jiji la Hebroni,+ katika eneo lenye milima la Yuda, na malisho yake yote. 12 Lakini walikuwa wamempa Kalebu mwana wa Yefune mashamba ya jiji hilo na vijiji vyake kuwa urithi wake.+
13 Nao wakawapa wana wa kuhani Haruni jiji la makimbilio kwa ajili ya muuaji,+ yaani, jiji la Hebroni,+ na malisho yake, pia Libna+ na malisho yake, 14 Yatiri+ na malisho yake, Eshtemoa+ na malisho yake, 15 Holoni+ na malisho yake, Debiri+ na malisho yake, 16 Aini+ na malisho yake, Yuta+ na malisho yake, na Beth-shemeshi na malisho yake—majiji tisa katika maeneo ya makabila hayo mawili.
17 Na katika eneo la kabila la Benjamini: Gibeoni+ na malisho yake, Geba na malisho yake,+ 18 Anathothi+ na malisho yake, na Almoni na malisho yake—majiji manne.
19 Wazao wa Haruni, makuhani, walipewa jumla ya majiji 13 na malisho yake.+
20 Na Walawi waliobaki wa koo za Wakohathi walipewa majiji kwa kura katika eneo la kabila la Efraimu. 21 Waliwapa jiji la makimbilio kwa ajili ya muuaji,+ yaani, jiji la Shekemu+ na malisho yake katika eneo lenye milima la Efraimu, Gezeri+ na malisho yake, 22 Kibsaimu na malisho yake, na Beth-horoni+ na malisho yake—majiji manne.
23 Na katika eneo la kabila la Dani: Elteke na malisho yake, Gibethoni na malisho yake, 24 Aiyaloni+ na malisho yake, Gath-rimoni na malisho yake—majiji manne.
25 Na katika eneo la nusu ya kabila la Manase: Taanaki+ na malisho yake na Gath-rimoni na malisho yake—majiji mawili.
26 Koo zilizobaki za Wakohathi zilipewa jumla ya majiji kumi na malisho yake.
27 Na Wagershoni+ wa koo za Walawi walipewa jiji la makimbilio kwa ajili ya muuaji katika eneo la nusu ya kabila la Manase, yaani, jiji la Golani+ kule Bashani pamoja na malisho yake, na Beeshtera na malisho yake—majiji mawili.
28 Na katika eneo la kabila la Isakari:+ Kishioni na malisho yake, Daberathi+ na malisho yake, 29 Yarmuthi na malisho yake, na En-ganimu na malisho yake—majiji manne.
30 Na katika eneo la kabila la Asheri:+ Mishali na malisho yake, Abdoni na malisho yake, 31 Helkathi+ na malisho yake, na Rehobu+ na malisho yake—majiji manne.
32 Na katika eneo la kabila la Naftali: jiji la makimbilio+ kwa ajili ya muuaji, yaani, jiji la Kedeshi+ kule Galilaya na malisho yake, Hamoth-dori na malisho yake, na Kartani na malisho yake—majiji matatu.
33 Wagershoni walipewa jumla ya majiji 13 na malisho yake kulingana na koo zao.
34 Na koo za Wamerari,+ yaani, Walawi waliobaki, walipewa Yokneamu+ na malisho yake, Karta na malisho yake, katika eneo la kabila la Zabuloni,+ 35 Dimna na malisho yake, na Nahalali+ na malisho yake—majiji manne.
36 Na katika eneo la kabila la Rubeni: Beseri+ na malisho yake, Yahazi na malisho yake,+ 37 Kedemothi na malisho yake, na Mefaathi na malisho yake—majiji manne.
38 Na katika eneo la kabila la Gadi:+ jiji la makimbilio kwa ajili ya muuaji, yaani, jiji la Ramothi kule Gileadi+ na malisho yake, Mahanaimu+ na malisho yake, 39 Heshboni+ na malisho yake, Yazeri+ na malisho yake—jumla ya majiji manne.
40 Majiji yote ambayo Wamerari walipewa kwa kura kulingana na koo zao, yaani, koo zilizobaki za Walawi, yalikuwa majiji 12.
41 Majiji yote ambayo Walawi walipewa katika maeneo ya Waisraeli yalikuwa majiji 48 pamoja na malisho yake.+ 42 Kila moja la majiji hayo lilizungukwa na malisho—hivyo ndivyo ilivyokuwa katika majiji hayo yote.
43 Basi Yehova akawapa Waisraeli nchi yote ambayo aliapa kwamba angewapa mababu zao,+ wakaimiliki na kuishi humo.+ 44 Yehova akawapa pia amani katika nchi yote, kama alivyowaapia mababu zao,+ na hakuna adui hata mmoja kati ya maadui wao wote aliyeweza kuwashinda.+ Yehova aliwatia maadui wao wote mikononi mwao.+ 45 Hakuna ahadi hata moja iliyokosa kutimia kati ya ahadi zote nzuri ambazo Yehova aliwaahidi Waisraeli; zote zilitimia.+
22 Kisha Yoshua akawaita watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase 2 na kuwaambia: “Mmefanya mambo yote ambayo Musa mtumishi wa Yehova aliwaamuru mfanye,+ nanyi mmetii sauti yangu kwa kufanya mambo yote niliyowaamuru.+ 3 Hamjawaacha ndugu zenu kwa muda wote huo, mpaka leo hii;+ nanyi mmetimiza wajibu wa kushika amri ya Yehova Mungu wenu.+ 4 Na Yehova Mungu wenu amewapumzisha ndugu zenu kama alivyowaahidi.+ Basi sasa rudini kwenye mahema yenu katika nchi ambayo Musa mtumishi wa Yehova aliwapa ng’ambo ya* Yordani.+ 5 Lakini muwe waangalifu sana kutekeleza amri na Sheria ambayo Musa mtumishi wa Yehova aliwapa,+ kwa kumpenda Yehova Mungu wenu,+ kutembea katika njia zake zote,+ kushika amri zake,+ kushikamana naye,+ na kumtumikia+ kwa moyo wenu wote na nafsi* yenu yote.”+
6 Basi Yoshua akawabariki na kuwaambia waende zao, nao wakarudi katika mahema yao. 7 Musa alikuwa ameipa nusu ya kabila la Manase urithi kule Bashani,+ na Yoshua akaipa nusu iliyobaki ya kabila hilo nchi upande wa magharibi wa Yordani,+ pamoja na ndugu zao. Zaidi ya hilo, Yoshua alipowaambia warudi katika mahema yao, aliwabariki 8 na kuwaambia: “Rudini katika mahema yenu mkiwa na utajiri mwingi, mifugo mingi sana, fedha na dhahabu, shaba na chuma, na mavazi mengi sana.+ Gawaneni na ndugu zenu nyara mlizochukua+ kutoka kwa maadui wenu.”
9 Kisha watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase wakawaacha Waisraeli wengine huko Shilo katika nchi ya Kanaani, wakarudi Gileadi,+ nchi yao ya urithi waliyokuwa wakiimiliki kama Yehova alivyowaagiza kupitia Musa.+ 10 Watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase walipofika maeneo ya Yordani katika nchi ya Kanaani, walijenga madhabahu karibu na Mto Yordani, madhabahu kubwa inayovutia. 11 Baadaye Waisraeli wengine wakasikia habari hizo+ na kusema, “Watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase wamejenga madhabahu kwenye mpaka wa nchi ya Kanaani katika maeneo ya Yordani ambayo ni ya Waisraeli.” 12 Waisraeli waliposikia habari hizo, wakakusanyika wote Shilo+ ili waende kupigana nao.
13 Kisha Waisraeli wakamtuma Finehasi+ mwana wa kuhani Eleazari kwa watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase katika nchi ya Gileadi, 14 na wakuu kumi walikuwa pamoja naye, mkuu mmoja kwa ajili ya kila ukoo* katika makabila yote ya Israeli, kila mmoja wao alikuwa kiongozi wa ukoo wake* miongoni mwa maelfu ya* Israeli.+ 15 Walipofika kwa watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase katika nchi ya Gileadi, wakawaambia:
16 “Kusanyiko lote la Yehova linasema hivi: ‘Mnawezaje kukosa uaminifu kwa Mungu wa Israeli kwa kufanya jambo kama hili?+ Leo, mmeacha kumfuata Yehova kwa kujijengea madhabahu na kumwasi Yehova.+ 17 Je, dhambi tuliyotenda kule Peori haikutosha? Mpaka leo hatujajitakasa kutokana nayo hata ingawa kusanyiko la Yehova lilipata pigo.+ 18 Na sasa mnaacha kumfuata Yehova! Mkimwasi Yehova leo, kesho atawakasirikia Waisraeli wote.+ 19 Basi ikiwa mnaona nchi mliyorithi si safi, vukeni na kuingia katika nchi ya Yehova+ ambayo ina hema la ibada+ ya Yehova mkae kati yetu, lakini msimwasi Yehova, wala msitufanye tuwe waasi kwa kujijengea madhabahu nyingine zaidi ya madhabahu ya Yehova Mungu wetu.+ 20 Akani+ mwana wa Zera alipokosa uaminifu na kuchukua kitu kilichopaswa kuharibiwa, je, Mungu hakuwakasirikia Waisraeli wote?+ Akani hakufa peke yake kwa sababu ya dhambi yake.’”+
21 Ndipo watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase wakawajibu hivi viongozi wa maelfu* katika Israeli:+ 22 “Mungu wa miungu, Yehova!* Mungu wa miungu, Yehova!+ Anajua, na Waisraeli pia watajua. Ikiwa tuliasi na kukosa uaminifu kwa Yehova, msituache hai leo. 23 Ikiwa tulijijengea madhabahu ili tuache kumfuata Yehova na kutoa juu yake dhabihu za kuteketezwa, matoleo ya nafaka, na dhabihu za ushirika, Yehova atatuadhibu.+ 24 Lakini hatukuijenga kwa sababu hiyo, tuliijenga kwa sababu tulisema, ‘Wakati ujao wana wenu watawauliza wana wetu: “Mna haki gani ya kumwabudu* Yehova Mungu wa Israeli? 25 Yehova ameweka Mto Yordani kuwa mpaka kati yetu na ninyi, watu wa kabila la Rubeni na Gadi. Hamna ushirika wowote na Yehova.” Na wana wenu watawazuia wana wetu kumwabudu* Yehova.’
26 “Basi tukasema, ‘Kwa vyovyote vile, tujenge madhabahu, lakini si kwa ajili ya matoleo au dhabihu za kuteketezwa, 27 bali iwe ushahidi kati yetu na ninyi+ na wazao wetu* kwamba tutamtumikia Yehova kwa dhabihu zetu za kuteketezwa, na matoleo yetu, na dhabihu zetu za ushirika,+ ili wana wenu wasiwaambie hivi wana wetu wakati ujao: “Hamna ushirika wowote na Yehova.”’ 28 Basi tukasema, ‘Wakituambia hivyo sisi na wazao wetu* wakati ujao, tutawajibu: “Angalieni mfano wa madhabahu ya Yehova ambayo mababu zetu walijenga, si kwa ajili ya matoleo au dhabihu za kuteketezwa, bali iwe ushahidi kati yetu na ninyi.”’ 29 Hatuwezi kamwe kuwazia kumwasi Yehova na kuacha kumfuata+ Yehova kwa kujenga madhabahu nyingine kwa ajili ya dhabihu za kuteketezwa, matoleo ya nafaka, na matoleo mengine, zaidi ya madhabahu ya Yehova Mungu wetu ambayo iko mbele ya hema lake la ibada!”+
30 Basi kuhani Finehasi, wakuu wa Waisraeli, na viongozi wa maelfu* katika Israeli waliokuwa pamoja naye waliposikia maneno yaliyosemwa na wazao wa Rubeni, Gadi, na Manase, wakaridhika.+ 31 Ndipo Finehasi mwana wa kuhani Eleazari akawaambia wazao wa Rubeni, Gadi, na Manase: “Leo tunajua kwamba Yehova yuko kati yetu kwa sababu hamjakosa uaminifu kwa Yehova katika jambo hili. Sasa mmewaokoa Waisraeli kutoka mikononi mwa Yehova.”
32 Baada ya Finehasi mwana wa kuhani Eleazari na wale wakuu kukutana na watu wa kabila la Rubeni na Gadi katika nchi ya Gileadi wakarudi katika nchi ya Kanaani na kuwaambia Waisraeli wengine habari hizo. 33 Na Waisraeli wakaridhika na habari hizo. Wakamsifu Mungu na kuacha mipango ya kupigana na watu wa kabila la Rubeni na Gadi na kuiharibu nchi yao.
34 Watu wa kabila la Rubeni na Gadi wakaipa jina madhabahu* hiyo, kwa sababu walisema “ni ushahidi kati yetu kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli.”
23 Siku nyingi baada ya Yehova kuwapa Waisraeli amani+ kwa kuwaokoa kutoka kwa maadui wote waliowazunguka, Yoshua alipokuwa amezeeka na umri wake kusonga sana,+ 2 Yoshua aliwaita Waisraeli wote,+ wazee wao, viongozi wao, waamuzi wao, na wakuu wao,+ akawaambia hivi: “Nimezeeka na umri wangu umesonga sana. 3 Ninyi wenyewe mmeona mambo yote ambayo Yehova Mungu wenu aliyatendea mataifa haya yote kwa ajili yenu, kwa sababu Yehova Mungu wenu ndiye aliyekuwa akiwapigania.+ 4 Tazameni, niliwagawia kwa kura+ nchi ya mataifa yanayobaki na pia nchi ya mataifa yote ambayo niliyaangamiza+ ili iwe urithi wa makabila yenu,+ kuanzia Yordani mpaka Bahari Kuu* upande wa magharibi. 5 Na Yehova Mungu wenu ndiye aliyekuwa akiwafukuza kutoka mbele yenu,+ naye akawaondoa* kwa ajili yenu, nanyi mkamiliki nchi yao, kama Yehova Mungu wenu alivyowaahidi.+
6 “Basi iweni jasiri sana mshike na kutekeleza mambo yote yaliyoandikwa katika kitabu cha Sheria+ ya Musa, msiiache kamwe na kwenda kulia wala kushoto,+ 7 na msishirikiane kamwe na mataifa haya+ yaliyobaki kati yenu. Hampaswi hata kutaja majina ya miungu yao+ wala kuapa kwa majina hayo, na hampaswi kamwe kuiabudu au kuiinamia.+ 8 Bali mnapaswa kushikamana na Yehova Mungu wenu,+ kama vile ambavyo mmekuwa mkifanya mpaka sasa. 9 Yehova atafukuza mataifa makubwa na yenye nguvu kutoka mbele yenu,+ kwa kuwa mpaka sasa hakuna mtu yeyote ambaye amewashinda ninyi.+ 10 Mtu mmoja tu kati yenu atawakimbiza watu elfu,+ kwa sababu Yehova Mungu wenu anawapigania,+ kama alivyowaahidi.+ 11 Basi jilindeni daima*+ kwa kumpenda Yehova Mungu wenu.+
12 “Lakini mkimwacha na kushikamana na watu wa mataifa haya yaliyobaki+ na kuoana nao+ na kushirikiana nao, 13 mjue kwa hakika kwamba Yehova Mungu wenu hataendelea kuyafukuza* mataifa haya kwa ajili yenu.+ Yatakuwa mtego wa kuwanasa, nayo yatakuwa mjeledi wa kuwachapa mbavuni+ na miiba machoni mwenu mpaka mtakapoangamia kutoka katika nchi hii nzuri ambayo Yehova Mungu wenu amewapa.
14 “Basi sasa nakaribia kufa,* nanyi mnajua vizuri kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi* zenu zote kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya ahadi zote nzuri ambazo Yehova Mungu wenu aliwaahidi. Zote zimetimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja aliloahidi.+ 15 Lakini kama zilivyotimia ahadi zote nzuri alizowaahidi Yehova Mungu wenu,+ vivyo hivyo Yehova atawaletea misiba yote aliyoahidi* na kuwaangamiza kutoka katika nchi hii nzuri ambayo Yehova Mungu wenu amewapa.+ 16 Mkivunja agano la Yehova Mungu wenu alilowaamuru mshike na mkienda kuabudu miungu mingine na kuiinamia, hasira ya Yehova itawaka dhidi yenu+ nanyi mtaangamia haraka kutoka katika nchi nzuri ambayo amewapa.”+
24 Kisha Yoshua akayakusanya makabila yote ya Israeli huko Shekemu, akawaita wazee wote wa Israeli, viongozi wao, waamuzi wao, na wakuu wao,+ nao wakasimama mbele za Mungu wa kweli. 2 Yoshua akawaambia watu wote, “Hivi ndivyo anavyosema Yehova Mungu wa Israeli, ‘Zamani za kale+ mababu zenu,+ kutia ndani Tera baba ya Abrahamu na baba ya Nahori, waliishi ng’ambo ya Mto,* nao walikuwa wakiabudu miungu mingine.+
3 “‘Baada ya muda nilimtoa babu yenu Abrahamu+ ng’ambo ya Mto* na kumtembeza katika nchi yote ya Kanaani na kuzidisha uzao wake.*+ Nikampa Isaka;+ 4 naye Isaka nikampa Yakobo na Esau.+ Baadaye nikampa Esau Mlima Seiri ili aumiliki;+ na Yakobo na wanawe wakashuka Misri.+ 5 Baadaye niliwatuma Musa na Haruni,+ nikailetea Misri mapigo,+ kisha nikawatoa ninyi. 6 Nilipokuwa nikiwatoa mababu zenu Misri,+ mlifika baharini, Wamisri waliwafuatia wakiwa na magari ya vita na askari wapanda farasi mpaka kwenye Bahari Nyekundu.*+ 7 Na mababu zenu wakaanza kumlilia Yehova,+ basi akaweka giza kati yenu na Wamisri na kuileta bahari juu yao ikawafunika Wamisri,+ na mliona kwa macho yenu wenyewe mambo niliyoyafanya huko Misri.+ Kisha mkaishi nyikani kwa miaka mingi.*+
8 “‘Nami nikawaleta katika nchi ya Waamori waliokuwa wakiishi ng’ambo ya* Yordani, nao wakapigana nanyi.+ Lakini niliwatia mikononi mwenu ili mmiliki nchi yao, nikawaangamiza kutoka mbele yenu.+ 9 Kisha Balaki mwana wa Sipori, mfalme wa Moabu, akaja kupigana na Israeli. Basi akamwita Balaamu mwana wa Beori ili awalaani ninyi.+ 10 Lakini sikumsikiliza Balaamu.+ Basi akawabariki ninyi tena na tena,+ nami nikawaokoa kutoka mikononi mwake.+
11 “‘Kisha mkavuka Yordani+ na kufika Yeriko.+ Nao viongozi* wa Yeriko, Waamori, Waperizi, Wakanaani, Wahiti, Wagirgashi, Wahivi, na Wayebusi wakapigana nanyi, lakini nikawatia mikononi mwenu.+ 12 Basi nikawafanya wavunjike moyo* kabla ya ninyi kufika, nao wakakimbia+—wafalme wawili wa Waamori. Hamkuwashinda kwa sababu ya upanga wenu wala upinde wenu.+ 13 Kwa hiyo niliwapa nchi ambayo hamkuipata kwa jasho lenu na majiji ambayo hamkujenga,+ nanyi mkakaa humo. Mnakula matunda ya mizabibu na ya mizeituni ambayo hamkupanda.’+
14 “Kwa hiyo, mwogopeni Yehova na kumtumikia kwa utimilifu* na uaminifu,*+ ondoeni miungu ambayo mababu zenu waliabudu ng’ambo ya Mto* na nchini Misri,+ nanyi mtumikieni Yehova. 15 Sasa ikiwa mnaona ni vibaya kumtumikia Yehova, chagueni leo yule mtakayemtumikia,+ iwe ni miungu ambayo mababu zenu waliabudu ng’ambo ya Mto*+ au miungu ya Waamori mnaoishi katika nchi yao.+ Lakini mimi na familia* yangu, tutamtumikia Yehova.”
16 Ndipo watu wakajibu hivi: “Hatuwezi kamwe kuwazia kumwacha Yehova na kuabudu miungu mingine. 17 Yehova Mungu wetu ndiye aliyetutoa sisi na mababu zetu katika nchi ya Misri,+ katika nyumba ya utumwa,+ na kufanya miujiza mikubwa mbele ya macho yetu+ na kutulinda katika safari yetu yote na miongoni mwa watu wote ambao tulipita katikati yao.+ 18 Yehova aliyafukuza mataifa yote, kutia ndani Waamori, walioishi katika nchi hii kabla yetu. Kwa hiyo, sisi pia tutamtumikia Yehova, kwa sababu yeye ni Mungu wetu.”
19 Kisha Yoshua akawaambia watu, “Hamwezi kumtumikia Yehova, kwa maana yeye ni Mungu mtakatifu;+ ni Mungu anayetaka watu wamwabudu yeye peke yake.+ Hatawasamehe uasi wenu na dhambi zenu.+ 20 Mkimwacha Yehova na kuabudu miungu ya kigeni, yeye pia atawaacha na kuwaangamiza hata ingawa amewatendea mema.”+
21 Lakini watu wakamwambia hivi Yoshua: “Hapana, tutamtumikia Yehova!”+ 22 Basi Yoshua akawaambia, “Ninyi ni mashahidi dhidi yenu wenyewe kwamba mmechagua kwa hiari yenu kumtumikia Yehova.”+ Nao wakajibu, “Sisi ni mashahidi.”
23 “Basi, ondoeni miungu ya kigeni iliyo kati yenu, mwelekeze mioyo yenu kwa Yehova Mungu wa Israeli.” 24 Watu wakamwambia Yoshua, “Tutamtumikia Yehova Mungu wetu, nasi tutaitii sauti yake!”
25 Kwa hiyo Yoshua akafanya agano na Waisraeli siku hiyo, akawapa maagizo na sheria huko Shekemu. 26 Kisha Yoshua akaandika maneno hayo katika kitabu cha Sheria+ ya Mungu, akachukua jiwe kubwa+ na kuliweka chini ya mti mkubwa kando ya mahali patakatifu pa Yehova.
27 Ndipo Yoshua akawaambia watu wote, “Tazameni! Jiwe hili litakuwa ushahidi dhidi yetu,+ kwa sababu limesikia maneno yote ambayo Yehova ametuambia, nalo litakuwa ushahidi dhidi yenu, ili msimkane Mungu wenu.” 28 Basi Yoshua akawaruhusu watu waende zao, nao wakaenda kila mtu kwenye urithi wake.+
29 Baada ya mambo hayo, Yoshua mwana wa Nuni, mtumishi wa Yehova, akafa akiwa na umri wa miaka 110.+ 30 Basi wakamzika kwenye eneo lake la urithi kule Timnath-sera,+ katika eneo lenye milima la Efraimu, upande wa kaskazini wa Mlima Gaashi. 31 Waisraeli waliendelea kumtumikia Yehova siku zote za Yoshua na sikuzote za wazee walioendelea kuishi baada ya Yoshua kufa ambao walikuwa wameona mambo yote makuu ambayo Yehova aliwatendea Waisraeli.+
32 Na mifupa ya Yosefu,+ ambayo Waisraeli walikuwa wameleta kutoka Misri, wakaizika huko Shekemu katika shamba ambalo Yakobo alinunua kwa vipande 100 vya fedha+ kutoka kwa wana wa Hamori,+ baba ya Shekemu; nalo likawa urithi wa wana wa Yosefu.+
33 Pia, Eleazari mwana wa Haruni akafa.+ Wakamzika katika Kilima cha Finehasi mwanawe,+ alichopewa katika eneo lenye milima la Efraimu.
Au “Yehoshua,” maana yake “Yehova Ni Wokovu.”
Yaani, Mediterania.
Au “kuelekea machweo ya jua.”
Au “ukitafakari.”
Yaani, upande wa mashariki.
Au “Bahari ya Shamu.”
Yaani, upande wa mashariki wa.
Tnn., “mioyo yetu iliyeyuka.”
Au “inayotegemeka.”
Au “mtaokoa nafsi zetu.”
Tnn., “Nafsi zetu zitakufa badala ya nafsi zenu!”
Tnn., “wana wote wa Israeli.”
Karibu mita 890 (futi 2,920). Angalia Nyongeza B14.
Au “ukuta.”
Au “ukuta.”
Tnn., “wana.”
Tnn., “wakamwogopa.”
Au “Bahari ya Shamu.”
Tnn., “upande unaoelekea baharini.”
Tnn., “mioyo yao ikayeyuka.”
Maana yake “Kilima cha Magovi.”
Au “wanaume wote wenye umri wa kwenda vitani.”
Maana yake “Kuondoa; Kuondolea Mbali.”
Au “kiongozi.”
Au “pembe zikipigwa kwa muda mrefu.”
Au “shida; laana.”
Au labda, “aliwaapisha watu kiapo.”
Maana yake “Machimbo.”
Tnn., “mioyo ya watu ikayeyuka.”
Yaani, upande wa mashariki wa.
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”
Au “shida; laana.”
Maana yake “Msiba; Laana.”
Au “nchi tambarare ya chini.”
Tnn., “waliotembea.”
Yaani, Mediterania.
Au “watumwa.”
Yaani, upande wa mashariki wa.
Au “wakakagua.”
Tnn., “tumo mikononi mwako.”
Tnn., “Usiulegeze mkono wako kutuelekea.”
Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”
Tnn., “kunoa ulimi wake.”
Au “nafsi yoyote iliyobaki.”
Tnn., “nafsi zote.”
Au “kila nafsi.”
Au “Araba.”
Au “Wakaziangamiza nafsi zote.”
Au “maeneo yake yaliyo chini ya milima.”
Au “Korongo.”
Au “Korongo.”
Yaani, Ziwa Genesareti, au Bahari ya Galilaya.
Au “hamjateka.”
Au “kijito cha Shihori.”
Au “mbele ya.”
Au “njia ya kuingia Hamathi.”
Au “Nitachukua nchi yao.”
Au “Korongo.”
Au “kuchukua nchi yao.”
Au “hawakuchukua nchi ya.”
Au “Korongo.”
Au “nchi tambarare ya chini.”
Yaani, wafalme waliokuwa chini ya Sihoni.
Au “mwaguzi.”
Au “nchi tambarare ya chini.”
Yaani, Ziwa Genesareti, au Bahari ya Galilaya.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, upande wa mashariki wa.
Tnn., “neno kama lilivyokuwa moyoni mwangu.”
Tnn., “waliifanya mioyo ya watu iyeyuke.”
Tnn., “kikamilifu; kabisa.”
Au “inaelekea.”
Au “nitachukua nchi yao.”
Au “waligawiwa kwa kura.”
Yaani, Bahari Kuu, Mediterania.
Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”
Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”
Yaani, Mediterania.
Yaani, “baba ya Aksa.”
Au labda, “akapiga makofi akiwa juu ya punda ili kumwita baba yake.”
Au “eneo la Negebu.”
Yaani, “Chemchemi za Maji.”
Au labda, “Gedera na mazizi yake ya kondoo.”
Yaani, Mediterania.
Au “waligawiwa kwa kura.”
Yaani, upande wa mashariki wa.
Tnn., “upande wa kulia.”
Yaani, mpaka wa watu wa kabila la Manase au eneo la Manase.
Au “hawakuchukua nchi yao.”
Au “nchi tambarare ya chini.”
Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”
Tnn., “magari ya chuma.”
Tnn., “magari ya chuma.”
Au “Nchi Tambarare ya Chini.”
Au “korongoni.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Au “anayeua nafsi.”
Au “bila kujua.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, upande wa mashariki wa.
Angalia Kamusi.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Au “koo za.”
Au “koo.”
Au “Mungu Mkuu, Yehova.”
Tnn., “Mna nini na.”
Tnn., “kumwogopa.”
Tnn., “vizazi vyetu.”
Tnn., “vizazi vyetu.”
Au “koo.”
Maelezo haya yanaonyesha kwamba huenda madhabahu hiyo iliitwa Ushahidi au Ushuhuda.
Yaani, Mediterania.
Au “akachukua nchi yao.”
Au “lindeni nafsi zenu kwa uangalifu.”
Au “kuchukua nchi ya.”
Tnn., “Leo ninafuata njia ya dunia yote.”
Angalia Kamusi.
Au “mabaya yote.”
Yaani, Mto Efrati.
Yaani, Mto Efrati.
Tnn., “mbegu yake.”
Au “Bahari ya Shamu.”
Tnn., “siku nyingi.”
Yaani, upande wa mashariki wa.
Au labda, “wamiliki wa mashamba.”
Au labda, “waogope; watishike.”
Au “bila lawama.”
Au “ukweli.”
Yaani, Mto Efrati.
Yaani, Mto Efrati.
Au “nyumba.”