KULINGANA NA MARKO
1 Mwanzo wa habari njema kumhusu Yesu Kristo, Mwana wa Mungu: 2 Kama ilivyoandikwa katika nabii Isaya: “(Tazama! Ninamtuma mjumbe wangu mbele yako,* ili akutayarishie njia.)+ 3 Kuna mtu anayepaza sauti nyikani: ‘Tayarisheni njia ya Yehova!* Nyoosheni barabara zake.’”+ 4 Yohana Mbatizaji alikuwa nyikani, akiwahubiria watu wabatizwe ili kuonyesha kwamba wametubu na hivyo wasamehewe dhambi zao.+ 5 Watu katika eneo lote la Yudea na wakaaji wote wa Yerusalemu walimwendea, naye akawabatiza* katika Mto Yordani,+ nao wakaungama dhambi zao waziwazi. 6 Yohana alikuwa akivaa mavazi yaliyofumwa kwa manyoya ya ngamia na alijifunga mshipi wa ngozi kiunoni,+ na alikula nzige na asali ya mwituni.+ 7 Naye alihubiri akisema: “Baada yangu, kuna mtu mwenye nguvu kuliko mimi anayekuja, nami sistahili kuinama ili kufungua kamba za viatu vyake.+ 8 Niliwabatiza ninyi kwa maji, lakini yeye atawabatiza kwa roho takatifu.”+
9 Siku hizo Yesu alikuja kutoka Nazareti ya Galilaya, na Yohana akambatiza katika Yordani.+ 10 Mara tu alipotoka katika maji akaona mbingu zikifunguka na roho takatifu ikishuka juu yake kama njiwa.+ 11 Sauti ikasikika kutoka mbinguni ikisema: “Wewe ni Mwanangu, mpendwa; nimekukubali.”+
12 Mara moja roho ikamchochea kuingia nyikani. 13 Basi akakaa nyikani kwa siku 40, akijaribiwa na Shetani.+ Aliishi kati ya wanyama wa mwituni, lakini malaika walikuwa wakimhudumia.+
14 Baada ya Yohana kukamatwa, Yesu alienda Galilaya+ akihubiri habari njema ya Mungu+ 15 akisema: “Wakati uliowekwa umefika, na Ufalme wa Mungu umekaribia. Tubuni+ na muwe na imani katika habari njema.”
16 Alipokuwa akitembea kando ya Bahari ya Galilaya alimwona Simoni na Andrea ndugu yake+ wakishusha nyavu zao baharini,+ kwa maana walikuwa wavuvi.+ 17 Basi Yesu akawaambia: “Nifuateni, nami nitawafanya muwe wavuvi wa watu.”+ 18 Mara moja wakaziacha nyavu zao na kumfuata.+ 19 Yesu aliposonga mbele kidogo akawaona Yakobo na Yohana, wana wa Zebedayo, kwenye mashua wakitengeneza nyavu zao,+ 20 na bila kukawia akawaita. Nao wakamwacha baba yao Zebedayo katika mashua pamoja na wafanyakazi, kisha wakamfuata Yesu. 21 Wakaenda Kapernaumu.
Mara tu Sabato ilipoanza, akaingia katika sinagogi, akaanza kufundisha.+ 22 Nao wakashangazwa na njia yake ya kufundisha, kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye mamlaka, si kama waandishi.+ 23 Wakati huohuo, kulikuwa na mtu katika sinagogi lao aliyekuwa na roho mwovu, naye akasema kwa sauti kubwa: 24 “Kwa nini unatusumbua, wewe Yesu Mnazareti?+ Je, umekuja kutuangamiza? Ninajua wewe ni nani, Mtakatifu wa Mungu!”+ 25 Lakini Yesu akamkemea, akisema: “Nyamaza, na umtoke!” 26 Na yule roho mwovu, baada ya kumfanya mtu huyo agaegae na kupiga kelele kwa sauti kubwa, akamtoka. 27 Basi, watu wote wakashangaa sana na kuulizana: “Ni jambo gani hili? Ni fundisho jipya! Hata anawaamuru roho waovu kwa mamlaka, nao wanamtii!” 28 Basi habari kumhusu zikaenea upesi kila mahali katika eneo lote la Galilaya.
29 Ndipo wakatoka kwenye sinagogi na kwenda nyumbani kwa Simoni na Andrea wakiwa na Yakobo na Yohana.+ 30 Sasa mama mkwe wa Simoni+ alikuwa amelala akiugua homa, na mara moja wakamwambia Yesu kumhusu. 31 Yesu akamkaribia, akamshika mkono na kumwinua. Akapona homa, naye akaanza kuwahudumia.
32 Ilipofika jioni, jua lilipotua, watu wakaanza kumletea wote waliokuwa wagonjwa na waliokuwa na roho waovu;+ 33 na jiji lote lilikuwa limekusanyika mlangoni. 34 Basi akawaponya watu wengi waliokuwa na magonjwa mbalimbali,+ akafukuza roho wengi waovu, lakini hakuwaruhusu hao roho waovu waseme, kwa maana walijua yeye ni Kristo.*
35 Asubuhi na mapema, kulipokuwa bado na giza, akaamka na kutoka nje, akaenda mahali pasipo na watu, naye akaanza kusali.+ 36 Hata hivyo, Simoni na wenzake wakamtafuta sana, 37 na walipompata wakamwambia: “Kila mtu anakutafuta.” 38 Lakini akawaambia: “Twendeni mahali pengine, katika miji iliyo karibu, ili nihubiri huko pia, kwa maana nilikuja kwa kusudi hilo.”+ 39 Naye akaenda akihubiri katika masinagogi yao katika Galilaya yote na kuwafukuza roho waovu.+
40 Mtu fulani mwenye ukoma akamjia, akapiga magoti na kumwomba: “Ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.”+ 41 Ndipo akamsikitikia, akanyoosha mkono wake, akamgusa na kumwambia: “Ninataka! Takasika.”+ 42 Mara moja ule ukoma ukaisha, akawa safi. 43 Kisha akampa maagizo thabiti na mara moja akamwacha aende, 44 akamwambia: “Usimwambie jambo lolote mtu yeyote, bali nenda ukajionyeshe kwa kuhani na utoe vitu alivyoagiza Musa kwa ajili ya kutakaswa kwako,+ ili kuwa ushahidi kwao.”+ 45 Hata hivyo, baada ya kuondoka, mtu huyo akaanza kueneza habari hizo kila mahali, hivi kwamba Yesu hakuweza kuingia katika jiji lolote waziwazi, bali alikaa nje mahali pasipo na watu. Lakini watu walizidi kumjia kutoka kila upande.+
2 Hata hivyo, baada ya siku kadhaa Yesu akarudi tena Kapernaumu na watu wakasikia kwamba yuko nyumbani.+ 2 Basi watu wengi sana wakaja hivi kwamba hapakuwa na nafasi tena, hata mlangoni, naye akaanza kuwahubiria.+ 3 Wakamletea mtu aliyepooza, akiwa amebebwa na watu wanne.+ 4 Lakini kwa sababu ya umati, hawakuweza kumleta moja kwa moja kwa Yesu, basi baada ya kutoboa sehemu ya paa lililokuwa juu ya Yesu, wakamteremsha yule mtu aliyepooza, akiwa amelala juu ya kitanda.* 5 Yesu alipoona imani yao,+ akamwambia yule mtu aliyepooza: “Mwanangu, umesamehewa dhambi zako.”+ 6 Sasa baadhi ya waandishi waliokuwa wameketi hapo wakaanza kuwaza mioyoni mwao:+ 7 “Kwa nini mtu huyu anasema hivyo? Anakufuru. Ni nani anayeweza kusamehe dhambi isipokuwa Mungu peke yake?”+ 8 Lakini mara moja Yesu akatambua rohoni mwake kwamba walikuwa wakiwaza hivyo, basi akawaambia: “Kwa nini mnawaza mambo hayo katika mioyo yenu?+ 9 Ni jambo gani rahisi zaidi, kumwambia mtu huyu aliyepooza, ‘Umesamehewa dhambi zako,’ au kusema, ‘Simama, uchukue kitanda chako utembee’? 10 Lakini ili mjue kwamba Mwana wa binadamu+ ana mamlaka ya kusamehe dhambi duniani—”+ akamwambia yule mtu aliyepooza: 11 “Ninakuambia, Simama, chukua kitanda chako, uende nyumbani.” 12 Ndipo akasimama, na mara moja akachukua kitanda chake akatembea mbele yao wote na kwenda nje. Basi, wote wakashangaa, na kumtukuza Mungu wakisema: “Hatujawahi kamwe kuona jambo kama hilo.”+
13 Akaenda tena kando ya bahari; na umati ukamjia, naye akaanza kuwafundisha. 14 Alipokuwa akipita, akamwona Lawi mwana wa Alfayo akiwa ameketi kwenye ofisi ya kodi, akamwambia: “Njoo uwe mfuasi wangu.” Mara moja akasimama na kumfuata.+ 15 Baadaye alipokuwa akila* katika nyumba ya Lawi, wakusanya kodi wengi na watenda dhambi walikuwa wakila* pamoja na Yesu na wanafunzi wake, kwa maana wengi wao walikuwa wakimfuata.+ 16 Lakini waandishi wa Mafarisayo, walipoona akila na watenda dhambi na wakusanya kodi, wakaanza kuwauliza wanafunzi wake: “Je, yeye hula pamoja na wakusanya kodi na watenda dhambi?” 17 Aliposikia hilo, Yesu akawaambia: “Watu wenye nguvu hawahitaji daktari, lakini wagonjwa wanamhitaji. Sikuja kuwaita waadilifu, bali watenda dhambi.”+
18 Wanafunzi wa Yohana na Mafarisayo walikuwa na zoea la kufunga. Basi wakaja na kumuuliza Yesu: “Kwa nini wanafunzi wa Yohana na wanafunzi wa Mafarisayo hufunga, lakini wanafunzi wako hawafungi?”+ 19 Yesu akawajibu: “Rafiki za bwana harusi+ hawahitaji kufunga wanapokuwa naye, sivyo? Bwana harusi akiwa pamoja nao hawawezi kufunga. 20 Lakini siku zitakuja ambapo bwana harusi ataondolewa kwao,+ ndipo watakapofunga siku hiyo. 21 Hakuna mtu anayeshona kiraka cha kitambaa kipya juu ya vazi la nje la zamani. Akifanya hivyo, kitambaa kipya kitatoka kwenye vazi la zamani, nalo litararuka vibaya zaidi.+ 22 Pia, hakuna mtu anayeweka divai mpya katika viriba vya divai vilivyochakaa. Akifanya hivyo, divai itapasua ngozi ya viriba naye atapoteza divai pamoja na ngozi. Lakini divai mpya huwekwa katika viriba vipya vya divai.”
23 Alipokuwa akipita kwenye mashamba ya nafaka siku ya Sabato, wanafunzi wake wakaanza kukata masuke ya nafaka huku wakitembea.+ 24 Hivyo, Mafarisayo wakamwambia: “Tazama sasa! Kwa nini wanafanya jambo lisilo halali siku ya Sabato?” 25 Lakini akawaambia: “Je, hamjasoma alilofanya Daudi, wakati alipokuwa na uhitaji na yeye na wanaume waliokuwa pamoja naye walipohisi njaa?+ 26 Jinsi katika simulizi kuhusu mkuu wa makuhani Abiathari,+ Daudi alivyoingia katika nyumba ya Mungu na kula mikate ya toleo,* ambayo si halali kwa mtu yeyote kula isipokuwa makuhani,+ naye akawapa pia watu waliokuwa pamoja naye?” 27 Kisha akawaambia: “Sabato iliwekwa kwa ajili ya mwanadamu,+ bali si mwanadamu kwa ajili ya Sabato. 28 Basi, Mwana wa binadamu pia ndiye Bwana wa Sabato.”+
3 Yesu akaingia tena ndani ya sinagogi, na palikuwa na mtu aliyepooza mkono.+ 2 Basi walikuwa wakimwangalia sana waone kama atamponya mtu huyo siku ya Sabato, ili wamshtaki. 3 Akamwambia yule mtu aliyepooza mkono: “Simama uje hapa katikati.” 4 Kisha akawauliza: “Je, ni halali kufanya mema au kufanya mabaya siku ya Sabato, kuokoa uhai* au kuua?”+ Lakini wakanyamaza. 5 Akawatazama kwa hasira na kuhuzunika sana kwa sababu mioyo yao ilikuwa migumu,+ akamwambia mtu huyo: “Nyoosha mkono wako.” Akaunyoosha mkono wake, nao ukapona. 6 Ndipo Mafarisayo wakaenda nje na mara moja wakafanya mkutano pamoja na wafuasi wa chama cha Herode+ ili wamuue Yesu.
7 Lakini Yesu na wanafunzi wake wakaelekea baharini, na umati mkubwa kutoka Galilaya na Yudea ukamfuata.+ 8 Hata kutoka Yerusalemu, Idumea, ng’ambo ya Yordani, na maeneo ya Tiro na Sidoni, umati mkubwa ukamjia uliposikia kuhusu mambo mengi aliyokuwa akifanya. 9 Naye akawaambia wanafunzi wake wamletee mashua ndogo ili umati usimsonge. 10 Kwa sababu aliwaponya watu wengi, wote waliokuwa wagonjwa sana walikuwa wakimkaribia ili wamguse.+ 11 Hata roho waovu,+ kila mara walipomwona, walianguka mbele yake na kupaza sauti wakisema: “Wewe ndiye Mwana wa Mungu.”+ 12 Lakini mara nyingi aliwaagiza kwa kusisitiza wasimtangaze.+
13 Akapanda mlimani na kuwaita wale aliowataka,+ nao wakaja.+ 14 Akaanzisha* kikundi cha wanaume 12, ambao pia aliwaita mitume, nao wangefuatana naye, na angewatuma kuhubiri 15 na wangekuwa na mamlaka ya kufukuza roho waovu.+
16 Kile kikundi cha wanaume 12+ alichoanzisha* kilikuwa na Simoni, ambaye pia alimwita Petro,+ 17 Yakobo na Yohana wana wa Zebedayo (ambao pia aliwaita Boanerge, jina linalomaanisha “Wana wa Ngurumo”),+ 18 Andrea, Filipo, Bartholomayo, Mathayo, Tomasi, Yakobo mwana wa Alfayo, Thadayo, Simoni Mkananayo,* 19 na Yuda Iskariote, ambaye baadaye alimsaliti.
Kisha Yesu akaingia ndani ya nyumba, 20 na umati ukakusanyika tena, hivi kwamba hata hawakupata nafasi ya kula. 21 Lakini watu wake wa ukoo waliposikia hilo, wakaenda kumkamata, kwa maana walikuwa wakisema: “Amerukwa na akili.”+ 22 Pia, waandishi walioshuka kutoka Yerusalemu walikuwa wakisema: “Ana Beelzebuli,* naye anawafukuza roho waovu kwa nguvu za mtawala wa roho waovu.”+ 23 Kisha akawaita na kuzungumza nao kwa mifano: “Shetani anawezaje kumfukuza Shetani? 24 Ufalme ukigawanyika dhidi yake wenyewe, hauwezi kusimama;+ 25 na nyumba ikigawanyika dhidi yake yenyewe, haiwezi kusimama. 26 Pia, ikiwa Shetani anajipinga mwenyewe na amegawanyika, hawezi kusimama, bali ataangamia. 27 Kwa kweli, hakuna yeyote anayeweza kuingia ndani ya nyumba ya mtu mwenye nguvu na kuiba mali zake isipokuwa kwanza amfunge mtu huyo. Hapo ndipo atakapoweza kuipora nyumba yake. 28 Kwa kweli ninawaambia kwamba wanadamu watasamehewa mambo yote, hata ziwe dhambi gani au maneno ya kukufuru wanayosema. 29 Lakini yeyote anayekufuru roho takatifu hatasamehewa milele,+ bali atakuwa na hatia ya dhambi ya milele.”+ 30 Alisema hivyo kwa sababu walikuwa wakisema: “Ana roho mwovu.”+
31 Mama yake na ndugu zake+ wakaja na kusimama nje, wakamtuma mtu akamwite.+ 32 Kwa kuwa umati ulikuwa umeketi kumzunguka, wakamwambia: “Tazama! Mama yako na ndugu zako wako nje wanakuita.”+ 33 Lakini akawauliza: “Mama yangu na ndugu zangu ni nani?” 34 Akawatazama watu walioketi kumzunguka, akasema: “Tazama, mama yangu na ndugu zangu!+ 35 Yeyote anayefanya mapenzi ya Mungu, huyo ndiye ndugu yangu, dada yangu, na mama yangu.”+
4 Yesu akaanza tena kufundisha kando ya bahari, na umati mkubwa sana ukakusanyika karibu naye. Basi akapanda ndani ya mashua na kuketi humo mbali kidogo na ufuo, lakini umati wote ulikuwa kando ya bahari, ufuoni.+ 2 Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi kwa mifano,+ na alipokuwa akifundisha akasema:+ 3 “Sikilizeni. Tazama! Mpandaji alienda kupanda mbegu.+ 4 Alipokuwa akipanda, mbegu fulani zikaanguka kando ya barabara, ndege wakaja na kuzila. 5 Nyingine zikaanguka kwenye miamba, mahali pasipo na udongo mwingi, na mara moja zikachipuka kwa sababu udongo haukuwa na kina.+ 6 Lakini jua lilipochomoza, ziliungua na kunyauka kwa sababu hazikuwa na mizizi. 7 Mbegu nyingine zikaanguka kwenye miiba, nayo miiba ikakua na kuzisonga, nazo hazikuzaa matunda.+ 8 Lakini nyingine zikaanguka kwenye udongo mzuri, nazo zikakua na kuongezeka, zikaanza kuzaa matunda, mara 30, 60, na 100 zaidi.”+ 9 Kisha akaongezea kusema: “Yule aliye na masikio ya kusikiliza, na asikilize.”+
10 Alipokuwa peke yake, wale waliokuwa karibu naye pamoja na wale 12 wakaanza kumuuliza kuhusu mifano hiyo.+ 11 Akawaambia: “Ninyi mmepewa siri takatifu+ ya Ufalme wa Mungu, lakini kwa wale walio nje mambo yote yako katika mifano,+ 12 ili, ingawa wanatazama, watazame lakini wasione, na ingawa wanasikia, wasikie lakini wasielewe; wala wasigeuke na kusamehewa.”+ 13 Tena akawaambia: “Ikiwa hamwelewi mfano huo, basi mtaelewaje mifano mingine yote?
14 “Mpandaji hupanda neno.+ 15 Basi, hawa ndio wale walio kando ya barabara ambapo neno hupandwa; lakini mara tu wanapolisikia, Shetani huja+ na kuliondoa neno lililopandwa ndani yao.+ 16 Vivyo hivyo, hawa ndio wale waliopandwa kwenye miamba; mara tu wanapolisikia neno, wanalikubali kwa shangwe.+ 17 Hata hivyo, hawana mizizi ndani yao, bali wanaendelea kwa muda fulani; kisha mara tu wanapopata taabu au mateso kwa sababu ya lile neno, wanakwazika. 18 Bado kuna wengine ambao wamepandwa kwenye miiba. Hawa ndio wale wanaolisikia neno,+ 19 lakini mahangaiko+ ya mfumo huu wa mambo* na nguvu za udanganyifu za utajiri+ na tamaa+ za mambo mengine yote huingia na kulisonga neno, nalo halizai matunda. 20 Mwishowe, wale waliopandwa kwenye udongo mzuri ni wale wanaolisikiliza neno na kulipokea vizuri na kuzaa matunda—mara 30, 60, au 100 zaidi.”+
21 Akaendelea kuwaambia: “Je, taa huletwa na kuwekwa chini ya kikapu* au chini ya kitanda? Je, hailetwi na kuwekwa juu ya kinara cha taa?+ 22 Kwa maana hakuna jambo lolote lililofichwa ambalo halitafichuliwa; hakuna jambo lolote lililofunikwa kwa uangalifu ambalo halitafunuliwa.+ 23 Yeyote aliye na masikio ya kusikiliza, na asikilize.”+
24 Tena akawaambia: “Sikilizeni kwa makini mambo mnayosikia.+ Kwa kipimo mnachopima, ndicho mtakachopimiwa, ndiyo, mtaongezewa hata zaidi. 25 Kwa maana aliye na kitu ataongezewa,+ lakini yule asiye na kitu, hata kile alicho nacho kitachukuliwa.”+
26 Basi akaendelea kusema: “Kwa hiyo Ufalme wa Mungu ni kama vile mtu anapopanda mbegu kwenye udongo. 27 Yeye hulala usiku na kuamka mchana, nazo mbegu huota na kuwa ndefu—naye hajui jinsi zinavyokua. 28 Udongo wenyewe hutokeza mazao hatua kwa hatua, kwanza jani, kisha suke, mwishowe nafaka iliyokomaa ndani ya suke. 29 Lakini mimea inapokuwa tayari, yeye hutumia mundu, kwa sababu wakati wa kuvuna umefika.”
30 Akaendelea kusema: “Tutaufananisha Ufalme wa Mungu na nini, au tutatumia mfano gani kuufafanua? 31 Ni kama mbegu ya haradali, ambayo ilipopandwa katika udongo ilikuwa ndogo kuliko mbegu zote duniani.+ 32 Lakini baada ya kupandwa, humea na kuwa kubwa kuliko mboga nyingine zote na kutokeza matawi makubwa, hivi kwamba ndege wa angani hupata makao chini ya kivuli chake.”
33 Akitumia mifano+ mingi kama hiyo, aliwafundisha neno kwa kadiri walivyoweza kusikiliza. 34 Kwa kweli, hakuwa akizungumza nao bila mfano, lakini alipokuwa na wanafunzi wake faraghani aliwafafanulia mambo yote.+
35 Ilipofika jioni siku hiyo, akawaambia wanafunzi wake: “Tuvuke twende ng’ambo ya bahari.”+ 36 Baada ya kuuaga umati, wakaenda pamoja na Yesu katika mashua, kama alivyokuwa, na kulikuwa na mashua nyinginezo pamoja naye.+ 37 Dhoruba kali ya upepo ikaanza kuvuma, mawimbi yakaipiga mashua, hivi kwamba ikakaribia kuzama.+ 38 Lakini Yesu alikuwa kwenye tezi, akiwa amelalia mto. Basi wakamwamsha na kumwambia: “Mwalimu, je, hujali kwamba tunakaribia kuangamia?” 39 Ndipo akasimama, akaukemea upepo na kuiambia bahari: “Nyamaza! Tulia!”+ Upepo ukakoma, kukawa shwari kabisa. 40 Basi akawauliza: “Kwa nini mnaogopa sana?* Je, bado hamna imani?” 41 Lakini wakaogopa sana, nao wakaulizana: “Kwa kweli, mtu huyu ni nani, hivi kwamba upepo na bahari vinamtii?”+
5 Basi, wakafika ng’ambo ya bahari na kuingia katika eneo la Wagerasene.+ 2 Mara tu Yesu alipotoka kwenye mashua akakutana na mtu mwenye roho mwovu akitoka makaburini.* 3 Alikuwa akikaa makaburini, na kufikia wakati huo hakuna mtu yeyote aliyeweza kumfunga kabisa hata kwa mnyororo. 4 Alikuwa amefungwa mara nyingi kwa pingu na minyororo, lakini aliikata minyororo na kuzivunja pingu; na hakuna mtu aliyeweza kumzuia. 5 Sikuzote, usiku na mchana alikuwa akipaza sauti makaburini na milimani na kujikatakata kwa mawe. 6 Lakini alipomwona Yesu kwa mbali, alimkimbilia na kumwinamia.+ 7 Kisha akapaza sauti na kusema: “Kwa nini unanisumbua, Yesu, Mwana wa Mungu Aliye Juu Zaidi? Ninakuapisha kwa Mungu usinitese.”+ 8 Kwa maana Yesu alikuwa akimwambia: “Mtoke mtu huyu, wewe roho mwovu.”+ 9 Lakini Yesu akamuuliza: “Unaitwa nani?” Naye akamwambia: “Jina langu ni Kikosi, kwa sababu tuko wengi.” 10 Naye akamsihi sana Yesu asiwafukuze roho hao kutoka katika nchi hiyo.+
11 Sasa kulikuwa na nguruwe wengi+ wakila hapo mlimani.+ 12 Basi hao roho waovu wakamsihi: “Turuhusu tuingie ndani ya wale nguruwe.” 13 Naye akawaruhusu. Ndipo wale roho waovu wakatoka na kuingia ndani ya wale nguruwe, kisha lile kundi likatimua mbio, likaruka poromoko* na kuzama baharini. Walikuwa karibu 2,000, nao wakafa maji baharini. 14 Lakini wachungaji wa nguruwe hao wakakimbia wakapeleka habari jijini na mashambani, watu wakaja kuona kilichotukia.+ 15 Basi wakamjia Yesu, wakamwona yule mtu aliyekuwa na roho waovu, ambaye mwanzoni alikuwa na kile kikosi, akiwa ameketi, amevaa nguo, na akiwa na akili timamu, nao wakaogopa. 16 Pia, wale walioona tukio hilo wakawasimulia mambo yaliyompata mtu huyo aliyekuwa na roho waovu na kuhusu wale nguruwe. 17 Basi wakaanza kumsihi Yesu aondoke katika eneo lao.+
18 Alipokuwa akipanda mashua, yule mtu aliyekuwa na roho waovu akaanza kumsihi aende pamoja naye.+ 19 Hata hivyo, hakumruhusu, bali alimwambia: “Nenda nyumbani kwa watu wako wa ukoo, ukawaambie mambo yote ambayo Yehova* amekufanyia na jinsi alivyokuonyesha rehema.” 20 Mtu huyo akaenda zake akaanza kutangaza katika Dekapoli* mambo yote ambayo Yesu alimfanyia, na watu wote wakashangaa.
21 Baada ya Yesu kuvuka tena ng’ambo ya bahari kwa mashua, umati mkubwa ukakusanyika karibu naye alipokuwa kando ya bahari.+ 22 Sasa mmoja wa maofisa wasimamizi wa sinagogi, aliyeitwa Yairo akaja, na alipomwona Yesu, akaanguka miguuni pake.*+ 23 Akamsihi mara nyingi, akisema: “Binti yangu mdogo ni mgonjwa sana.* Tafadhali njoo uweke mikono yako juu yake+ ili apone na kuishi.” 24 Ndipo Yesu akaenda pamoja naye, na umati mkubwa ulikuwa ukimfuata na kumsonga.
25 Sasa kuna mwanamke aliyekuwa na mtiririko wa damu+ kwa miaka 12.+ 26 Alikuwa ameteseka sana* mikononi mwa madaktari wengi na alikuwa ametumia mali yake yote, na hakuwa amepona, badala yake hali yake ilizidi kuwa mbaya. 27 Aliposikia kumhusu Yesu, akapenya katika umati nyuma ya Yesu na kuligusa vazi lake la nje,+ 28 kwa maana alikuwa akisema: “Nikiyagusa tu mavazi yake ya nje, nitapona.”+ 29 Papo hapo mtiririko wake wa damu ukakoma, naye akahisi mwilini mwake kwamba alikuwa amepona ule ugonjwa mbaya.
30 Mara moja Yesu akahisi ndani yake kwamba nguvu+ zimemtoka, akaugeukia umati na kuuliza: “Ni nani aliyegusa mavazi yangu ya nje?”+ 31 Lakini wanafunzi wake wakamwambia: “Unaona jinsi umati unavyokusonga, na unauliza, ‘Ni nani aliyenigusa?’” 32 Hata hivyo, alikuwa akitazama ili aone mtu aliyekuwa amefanya hivyo. 33 Yule mwanamke akijua lililompata, akaja akitetemeka kwa hofu akaanguka chini mbele yake, akamwambia ukweli wote. 34 Yesu akamwambia: “Binti yangu, imani yako imekuponya. Nenda kwa amani,+ umepona ugonjwa wako mbaya.”+
35 Alipokuwa bado anazungumza, watu fulani kutoka nyumbani kwa yule ofisa msimamizi wa sinagogi wakaja na kusema: “Binti yako amekufa! Kwa nini uendelee kumsumbua Mwalimu?”+ 36 Lakini Yesu akasikia maneno yao naye akamwambia yule ofisa msimamizi wa sinagogi: “Usiogope, uwe tu na imani.”*+ 37 Hakumruhusu mtu yeyote amfuate isipokuwa Petro, Yakobo, na Yohana ndugu ya Yakobo.+
38 Wakafika kwenye nyumba ya yule ofisa msimamizi wa sinagogi, Yesu akaona mvurugo wa watu waliokuwa wakilia na kuomboleza kwa sauti kubwa.+ 39 Baada ya kuingia, akawaambia: “Kwa nini mnaomboleza na kuleta mvurugo? Mtoto hajafa bali amelala usingizi.”+ 40 Ndipo wakaanza kumcheka kwa dharau. Lakini baada ya kuwatoa wote nje, akamchukua baba na mama ya yule mtoto pamoja na wanafunzi wake, akaingia mahali alipokuwa huyo mtoto. 41 Kisha akaushika mkono wa msichana huyo na kumwambia: “Talitha kumi,” maneno ambayo yanapotafsiriwa, yanamaanisha: “Msichana mdogo, ninakuambia, ‘inuka!’”+ 42 Mara moja yule msichana akasimama akaanza kutembea. (Alikuwa na umri wa miaka 12.) Ndipo wakawa na shangwe kubwa sana. 43 Lakini akawaagiza tena na tena* wasimwambie mtu yeyote kuhusu jambo hilo,+ naye akawaambia wampe mtoto huyo chakula.
6 Akaondoka huko na kwenda kwenye eneo lake la nyumbani,+ na wanafunzi wake wakamfuata. 2 Ilipofika siku ya Sabato, akaanza kufundisha katika sinagogi, na wengi waliomsikiliza wakashangaa na kusema: “Mtu huyu alitoa wapi mambo haya?+ Kwa nini alipewa hekima hii, na kwa nini matendo haya yenye nguvu yafanywe kupitia mikono yake?+ 3 Je, huyu si yule seremala+ mwana wa Maria+ na ndugu ya Yakobo,+ Yosefu, Yuda, na Simoni?+ Na dada zake wapo hapa pamoja nasi, sivyo?” Basi wakaanza kukwazika kwa sababu yake. 4 Lakini Yesu akawaambia: “Nabii anaheshimiwa kila mahali isipokuwa katika eneo lake la nyumbani na kati ya watu wake wa ukoo, na katika nyumba yake mwenyewe.”+ 5 Basi, hakuweza kufanya matendo yoyote yenye nguvu huko isipokuwa kuweka mikono yake juu ya wagonjwa wachache na kuwaponya. 6 Kwa kweli, alishangaa sana kwa sababu hawakuwa na imani. Naye akaenda akizunguka vijijini, akifundisha.+
7 Sasa akawaita wale 12 akaanza kuwatuma wawili wawili,+ naye akawapa mamlaka juu ya roho waovu.+ 8 Pia, akawaagiza wasibebe chochote kwa ajili ya safari isipokuwa fimbo—wasibebe mkate, mfuko wa chakula, wala pesa* kwenye mishipi yao+— 9 bali wavae viatu lakini wasivae mavazi mawili.* 10 Pia, akawaambia: “Mtakapoingia katika nyumba yoyote, kaeni humo mpaka mtakapoondoka huko.+ 11 Na mahali popote ambapo watu hawatawakaribisha wala kuwasikiliza, mnapoondoka kung’uteni mavumbi yaliyo kwenye miguu yenu ili kuwa ushahidi kwao.”+ 12 Basi wakaondoka na kuhubiri kwamba watu wanapaswa kutubu,+ 13 pia wakafukuza roho wengi waovu+ na kuwapaka mafuta wagonjwa wengi na kuwaponya.
14 Mfalme Herode akasikia habari hizo, kwa maana jina la Yesu lilijulikana sana na watu walikuwa wakisema: “Yohana Mbatizaji amefufuliwa kutoka kwa wafu, ndiyo sababu anafanya matendo yenye nguvu.”+ 15 Lakini wengine walikuwa wakisema: “Ni Eliya.” Pia, wengine wakasema: “Ni nabii kama manabii wa kale.”+ 16 Lakini Herode alipopata habari hizo akasema: “Yule Yohana niliyemkata kichwa, amefufuliwa.” 17 Kwa maana Herode alikuwa ameagiza Yohana akamatwe na kufungwa gerezani kwa sababu ya Herodia, mke wa Filipo ndugu yake. Kwa sababu Herode alikuwa amemwoa.+ 18 Kwa maana Yohana alikuwa akimwambia Herode: “Si halali kwako kuwa na mke wa ndugu yako.”+ 19 Basi Herodia alikuwa na kinyongo kumwelekea Yohana na alitaka kumuua, lakini hakuweza. 20 Kwa maana Herode alimwogopa Yohana kwa kuwa alijua ni mtu mwadilifu na mtakatifu,+ naye alikuwa akimlinda. Baada ya kumsikiliza, hakujua la kufanya, lakini bado aliendelea kumsikiliza kwa furaha.
21 Nafasi ilipatikana Herode alipoandaa mlo wa jioni kwenye sherehe ya sikukuu yake ya kuzaliwa.+ Akawaalika maofisa wake wa cheo cha juu, makamanda wa jeshi, na watu mashuhuri zaidi wa Galilaya.+ 22 Binti ya Herodia akaingia, akacheza dansi na kumfurahisha Herode na wageni wake.* Mfalme akamwambia msichana huyo: “Niombe chochote unachotaka, nami nitakupa.” 23 Ndiyo, akamwapia: “Chochote utakachoomba nitakupa, hata ikiwa ni nusu ya ufalme wangu.” 24 Akaondoka na kwenda kumuuliza mama yake: “Niombe nini?” Akamwambia: “Kichwa cha Yohana Mbatizaji.” 25 Akarudi haraka mbele ya mfalme na kutoa ombi lake, akisema: “Nataka unipe sasa hivi kwenye sinia kichwa cha Yohana Mbatizaji.”+ 26 Ingawa mfalme alihuzunika sana, hakutaka kupuuza ombi lake, kwa sababu ya viapo vyake na wageni wake.* 27 Mara moja mfalme akamtuma mlinzi na kumwamuru alete kichwa cha Yohana. Basi akaenda gerezani na kumkata kichwa, 28 akakileta kwenye sahani. Akampa yule msichana, na huyo msichana akampa mama yake. 29 Wanafunzi wake waliposikia jambo hilo, wakaja na kuuchukua mwili wake wakaulaza kaburini.*
30 Mitume wakamzunguka Yesu na kumwambia mambo yote waliyokuwa wamefanya na kufundisha.+ 31 Naye akawaambia: “Twendeni faraghani mahali pasipo na watu ili mpumzike kidogo.”+ Kwa maana wengi walikuwa wakija na kwenda, nao hawakuwa na wakati hata wa kula. 32 Basi wakapanda mashua na kwenda mahali pasipo na watu ili wawe peke yao.+ 33 Lakini watu wakawaona wakienda na wengi wakajua jambo hilo. Watu kutoka majiji yote wakakimbia kwa miguu wakafika huko mbele yao. 34 Basi, aliposhuka, akaona umati mkubwa, akawasikitikia,+ kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji.+ Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.+
35 Ilipokaribia jioni wanafunzi wake wakaja na kumwambia: “Mahali hapa hapana watu, na muda umesonga sana.+ 36 Waambie waondoke, waende wakajinunulie chakula katika maeneo ya mashambani na vijiji vilivyo karibu.”+ 37 Akawajibu: “Ninyi wapeni chakula.” Nao wakamwambia: “Je, twende tukanunue mikate ya dinari* 200 na kuwapa watu wale?”+ 38 Akawaambia: “Mna mikate mingapi? Nendeni mkaangalie!” Baada ya kuhakikisha, wakasema: “Mikate mitano na samaki wawili.”+ 39 Akawaagiza watu wote waketi katika vikundi kwenye nyasi.+ 40 Basi wakaketi katika vikundi vya watu 100 na vya watu 50. 41 Akachukua ile mikate mitano na wale samaki wawili, akatazama mbinguni akatoa baraka.+ Kisha akaimega mikate na kuanza kuwapa wanafunzi ili wawape watu, naye akawagawanya wale samaki wawili kwa ajili ya watu wote. 42 Basi wote wakala wakashiba, 43 nao wakakusanya vipande vilivyobaki na kujaza vikapu 12, bila kuhesabu samaki.+ 44 Wale waliokula mikate hiyo walikuwa wanaume 5,000.
45 Kisha, bila kukawia, akawaagiza wanafunzi wake wapande mashua watangulie kuelekea Bethsaida ng’ambo ya bahari, huku yeye akiuaga umati.+ 46 Lakini baada ya kuwaaga, akaenda mlimani kusali.+ 47 Ilipofika jioni, mashua ilikuwa katikati ya bahari, lakini yeye alikuwa peke yake kwenye nchi kavu.+ 48 Alipowaona wanafunzi wake wakitaabika kupiga makasia kwa kuwa upepo ulikuwa ukivuma kinyume chao, usiku karibu kesha la nne* akawaendea akitembea juu ya bahari; lakini alitaka* kuwapita. 49 Walipomwona akitembea juu ya bahari wakafikiri: “Ni mzuka!” Nao wakapaza sauti. 50 Kwa maana wote walimwona, wakahangaika. Lakini mara moja akawaambia: “Jipeni moyo! Ni mimi; msiogope.”+ 51 Kisha akapanda kwenye mashua, na upepo ukatulia. Nao wakashangaa sana, 52 kwa maana hawakuwa wamefahamu maana ya ule muujiza wa mikate, bado mioyo yao ilikuwa mizito isiweze kuelewa.
53 Walipovuka bahari, wakafika Genesareti na kutia nanga hapo karibu.+ 54 Lakini mara tu waliposhuka kutoka kwenye mashua, watu wakamtambua. 55 Wakakimbia katika eneo hilo lote na kuanza kuleta wagonjwa wakiwa kwenye vitanda* mahali waliposikia Yesu yuko. 56 Na kila mahali alipokwenda katika vijiji, majiji, au mashambani watu waliwaweka wagonjwa sokoni, na kumsihi waguse tu upindo wa vazi lake la nje.+ Na wote waliougusa wakapona.
7 Sasa Mafarisayo na baadhi ya waandishi waliotoka Yerusalemu wakakusanyika kumzunguka Yesu.+ 2 Wakaona baadhi ya wanafunzi wake wakila chakula kwa mikono isiyo safi, yaani, bila kunawa.* 3 (Kwa maana kabla ya kula, Mafarisayo na Wayahudi wote hunawa mikono yao mpaka kwenye kiwiko, kwa kuyashika mapokeo ya mababu zao, 4 na wanapotoka sokoni, hawali chakula kabla ya kujisafisha. Kuna mapokeo mengine mengi ambayo wamepokea na kuyashika, kama vile kubatiza* vikombe, mitungi, na vyombo vya shaba.)+ 5 Basi Mafarisayo na waandishi hao wakamuuliza: “Kwa nini wanafunzi wako hawafuati mapokeo ya mababu zetu, bali wanakula kwa mikono isiyo safi?”+ 6 Akawaambia: “Isaya kwa kufaa alitoa unabii kuwahusu ninyi wanafiki, kama ilivyoandikwa, ‘Watu hawa huniheshimu kwa midomo yao, lakini mioyo yao iko mbali nami.+ 7 Wao huniabudu bure, kwa maana wanafundisha amri za wanadamu kuwa mafundisho.’+ 8 Mnaiacha amri ya Mungu, na kuyashika mapokeo ya wanadamu.”+
9 Akaendelea kuwaambia: “Mnapuuza amri ya Mungu kwa ujanja ili mfuate mapokeo yenu.+ 10 Kwa mfano, Musa alisema, ‘Mheshimu baba yako na mama yako,’+ na, ‘Yeyote anayemtukana* baba yake au mama yake anapaswa kuuawa.’+ 11 Lakini ninyi mnasema, ‘Mtu akimwambia baba yake au mama yake: “Chochote nilicho nacho ambacho kingekusaidia ni korbani, (yaani, zawadi iliyowekwa wakfu kwa Mungu),”’ 12 hivyo mnamzuia kumsaidia kwa chochote baba yake au mama yake.+ 13 Kwa hiyo, mnalibatilisha neno la Mungu kwa mapokeo yenu ambayo mlipewa.+ Nanyi mnafanya mambo mengine mengi kama hayo.”+ 14 Basi Yesu akauita tena umati, akawaambia: “Nisikilizeni, ninyi nyote, na mwelewe maana yake.+ 15 Mtu hawezi kuchafuliwa na kitu kinachoingia ndani yake; bali huchafuliwa na mambo yanayotoka ndani yake.”+ 16* ——
17 Alipouacha umati, Yesu aliingia ndani ya nyumba, na wanafunzi wake wakaanza kumuuliza kuhusu mfano huo.+ 18 Basi akawaambia: “Je, ninyi pia hamwelewi kama wao? Je, hamjui kwamba mtu hawezi kuchafuliwa na kitu kinachoingia ndani yake, 19 kwa kuwa hakiingii moyoni mwake bali huingia tumboni, kisha hutoka na kuingia chooni?” Kwa hiyo akatangaza vyakula vyote kuwa safi. 20 Tena akasema: “Kile kinachotoka ndani ya mtu ndicho humchafua.+ 21 Kwa maana kutoka ndani, moyoni mwa watu,+ hutoka mawazo mabaya: uasherati,* wizi, mauaji, 22 uzinzi, pupa, uovu, udanganyifu, mwenendo mpotovu,* jicho lenye wivu, makufuru, majivuno, na ukosefu wa akili. 23 Mambo hayo yote maovu hutoka ndani, nayo humchafua mtu.”
24 Akatoka huko na kwenda kwenye maeneo ya Tiro na Sidoni.+ Akaingia katika nyumba na hakutaka mtu yeyote ajue, lakini hakuweza kuepuka kutambuliwa. 25 Mara moja mwanamke ambaye binti yake mdogo alikuwa na roho mwovu akasikia kumhusu Yesu, akaja na kuanguka miguuni pake.+ 26 Mwanamke huyo alikuwa Mgiriki, wa taifa la* Sirofoinike; naye aliendelea kumsihi sana Yesu amfukuze roho mwovu aliyekuwa ndani ya binti yake. 27 Lakini Yesu akamwambia: “Kwanza acha watoto washibe, kwa maana haifai kuchukua mkate wa watoto na kuwatupia mbwa wadogo.”+ 28 Hata hivyo, yule mwanamke akamjibu: “Ndiyo, bwana, lakini hao mbwa wadogo walio chini ya meza hula makombo ya watoto wadogo.” 29 Ndipo Yesu akamwambia: “Kwa sababu umesema hivyo, nenda; yule roho mwovu amemtoka binti yako.”+ 30 Basi akaenda nyumbani akamkuta yule mtoto akiwa amelala kitandani, na yule roho mwovu alikuwa amemtoka.+
31 Yesu aliporudi kutoka eneo la Tiro akapitia Sidoni, Dekapoli,* na kufika Bahari ya Galilaya.+ 32 Basi wakamletea mtu aliye kiziwi na mwenye tatizo la kuzungumza,+ nao wakamsihi aweke mkono juu yake. 33 Kisha akampeleka faraghani, mbali na umati. Halafu akamtia vidole masikioni, baada ya kutema mate, akamgusa ulimi.+ 34 Yesu akatazama mbinguni, akavuta pumzi kwa nguvu na kumwambia: “Efatha,” yaani, “Funguka.” 35 Ndipo masikio yake yakafunguliwa,+ na tatizo lake la kuzungumza likaisha, naye akaanza kuzungumza vizuri. 36 Kisha akawaamuru wasimwambie mtu yeyote,+ lakini kadiri alivyowakataza, ndivyo walivyozidi kutangaza jambo hilo.+ 37 Kwa kweli, walishangaa sana+ wakasema: “Amefanya mambo yote vema. Hata anafanya viziwi wasikie na wasio na uwezo wa kusema, wazungumze.”+
8 Siku hizo umati mkubwa ukakusanyika tena, na hawakuwa na chakula. Basi, akawaita wanafunzi na kuwaambia: 2 “Ninausikitikia umati,+ kwa sababu tayari wamekaa pamoja nami siku tatu nao hawana chakula.+ 3 Nikiwaacha waende nyumbani wakiwa na njaa,* watazimia njiani, na baadhi yao wametoka mbali.” 4 Lakini wanafunzi wake wakamjibu: “Tutapata wapi mikate ya kuwatosha watu hawa mahali hapa pasipo na watu?” 5 Ndipo akawauliza: “Mna mikate mingapi?” Wakajibu: “Saba.”+ 6 Naye akauagiza umati uketi chini. Kisha akachukua ile mikate saba, akatoa shukrani, akaimega, na kuanza kuwapa wanafunzi wake waigawe, nao wakaugawia umati.+ 7 Walikuwa pia na samaki wachache wadogo, naye akawabariki, kisha akawaambia wawagawe hao pia. 8 Basi wakala wakashiba, kisha wakakusanya vipande vilivyobaki wakajaza vikapu saba vikubwa.+ 9 Kulikuwa na wanaume 4,000 hivi. Kisha Yesu akawaaga.
10 Mara moja akapanda mashua pamoja na wanafunzi wake akaenda eneo la Dalmanutha.+ 11 Akiwa huko Mafarisayo wakaja na kuanza kubishana naye, wakimtaka afanye ishara kutoka mbinguni, ili wamjaribu.+ 12 Kwa hiyo akahuzunika sana rohoni na kusema: “Kwa nini kizazi hiki kinatafuta ishara?+ Kwa kweli nasema, kizazi hiki hakitapewa ishara yoyote.”+ 13 Ndipo akawaacha, akapanda mashua tena na kuvuka ng’ambo ya bahari.
14 Hata hivyo, walisahau kuchukua mikate na walikuwa na mkate mmoja tu katika mashua.+ 15 Naye akawaonya waziwazi akisema: “Endeleeni kuwa macho; jihadharini na chachu* ya Mafarisayo na ya Herode.”+ 16 Basi wakaanza kubishana kati yao kwa sababu hawakuwa na mikate. 17 Yesu alipojua hilo, akawaambia: “Kwa nini mnabishana kuhusu kutokuwa na mikate? Je, bado hamjafahamu wala kuelewa? Je, bado mioyo yenu ni mizito isiweze kuelewa? 18 ‘Ingawa mna macho, kwa nini hamwoni; na ingawa mna masikio, kwa nini hamsikii?’ Je, hamkumbuki 19 nilipoimega ile mikate mitano+ kwa ajili ya wale wanaume 5,000, mlikusanya vipande vilivyobaki mkajaza vikapu vingapi?” Wakamwambia: “Kumi na viwili.”+ 20 “Nilipoimega ile mikate saba kwa ajili ya wale wanaume 4,000, mlikusanya vipande vilivyobaki mkajaza vikapu vikubwa vingapi?” Wakamwambia: “Saba.”+ 21 Ndipo akawauliza: “Je, bado hamjaelewa?”
22 Sasa wakafika Bethsaida. Watu wakamletea mwanamume aliye kipofu, wakamsihi amguse.+ 23 Yesu akamshika mkono yule kipofu, akampeleka nje ya kijiji. Kisha akamtemea mate machoni,+ akaweka mikono juu yake na kumuuliza: “Je, unaona kitu chochote?” 24 Yule mtu akatazama juu na kusema: “Ninaona watu, lakini wanaonekana kama miti inayotembea.” 25 Akaweka tena mikono yake juu ya macho ya mtu huyo, naye akaona vizuri. Akawa tena na uwezo wa kuona, naye alikuwa akiona kila kitu waziwazi. 26 Basi akamwacha aende nyumbani, na kumwambia: “Usiingie kijijini.”
27 Yesu na wanafunzi wake wakaelekea kwenye vijiji vya Kaisaria Filipi, na wakiwa njiani, Yesu akaanza kuwauliza wanafunzi wake: “Watu wanasema mimi ni nani?”+ 28 Wakamjibu: “Yohana Mbatizaji,+ lakini wengine Eliya,+ na bado wengine mmoja wa manabii.” 29 Naye akawauliza: “Hata hivyo, ninyi mnasema mimi ni nani?” Petro akajibu: “Wewe ndiye Kristo.”+ 30 Ndipo akawaamuru wasimwambie mtu yeyote kumhusu.+ 31 Pia, akaanza kuwafundisha kwamba Mwana wa binadamu lazima apatwe na mateso mengi na kukataliwa na wazee, wakuu wa makuhani, na waandishi, kisha atauawa,+ na baada ya siku tatu atafufuliwa.+ 32 Kwa kweli, alisema mambo hayo waziwazi. Lakini Petro akampeleka kando na kuanza kumkemea.+ 33 Yesu akageuka na kuwatazama wanafunzi wake, akamkemea Petro, akisema: “Nenda nyuma yangu, Shetani! kwa sababu hufikirii mawazo ya Mungu, bali ya wanadamu.”+
34 Sasa akauita umati na wanafunzi wake, akawaambia: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe, aubebe mti wake wa mateso* na aendelee kunifuata.+ 35 Kwa kuwa yeyote anayetaka kuokoa uhai wake ataupoteza,* lakini yeyote anayeupoteza uhai wake* kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema atauokoa.+ 36 Kwa kweli, mtu atapata faida gani akiupata ulimwengu wote kisha apoteze uhai wake?*+ 37 Kwa kweli, mtu anaweza kutoa nini ili abadilishane na uhai wake?*+ 38 Kwa maana yeyote atakayenionea aibu mimi na maneno yangu katika kizazi hiki chenye uzinzi * na chenye dhambi, Mwana wa binadamu atamwonea aibu pia+ atakapokuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu.”+
9 Yesu akaendelea kusema: “Kwa kweli ninawaambia kwamba kuna baadhi ya wale waliosimama hapa ambao hawataonja kifo kamwe kabla ya kuona Ufalme wa Mungu ukiwa tayari umekuja katika nguvu.”+ 2 Siku sita baadaye Yesu akaenda pamoja na Petro, Yakobo, na Yohana kwenye mlima mrefu wakiwa peke yao. Sura yake ikageuka mbele yao;+ 3 mavazi yake ya nje yakaanza kumetameta, yakawa meupe kuliko vile mfuaji nguo yeyote duniani angeweza kuyasafisha. 4 Pia, wakaona Eliya na Musa, wakizungumza na Yesu. 5 Kisha Petro akamwambia Yesu: “Rabi, ni vizuri sisi tuwe hapa. Basi, tutasimamisha mahema matatu, moja lako, moja la Musa, na moja la Eliya.” 6 Kwa kweli, hakujua afanye nini, kwa maana walikuwa wameogopa sana. 7 Wingu likatokea na kuwafunika, na sauti+ ikasikika kutoka katika lile wingu ikisema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa.+ Msikilizeni.”+ 8 Kisha ghafla wakatazama huku na huku na hawakumwona tena mtu yeyote isipokuwa Yesu.
9 Walipokuwa wakishuka kutoka mlimani, akawaamuru wasimwambie mtu yeyote kile walichoona,+ hadi Mwana wa binadamu atakapofufuliwa kutoka kwa wafu.+ 10 Wakayaweka maneno hayo moyoni,* lakini wakazungumza kati yao wenyewe kuhusu maana ya huko kufufuliwa kutoka kwa wafu. 11 Wakaanza kumuuliza: “Kwa nini waandishi husema kwamba lazima Eliya+ aje kwanza?”+ 12 Akawaambia: “Eliya anakuja kwanza na kurudisha mambo yote;+ lakini kwa nini imeandikwa kwamba lazima Mwana wa binadamu apatwe na mateso mengi+ na atendewe kwa dharau?+ 13 Lakini ninawaambia kwamba kwa kweli, Eliya+ amekuja nao walimtendea kama walivyotaka, kama ilivyoandikwa kumhusu.”+
14 Walipowakaribia wale wanafunzi wengine, wakaona umati mkubwa umewazunguka, na kulikuwa na waandishi waliokuwa wakibishana nao.+ 15 Lakini mara tu umati wote ulipomwona, ukashangaa, ukamkimbilia ili kumsalimu. 16 Basi akawauliza: “Mnabishania nini?” 17 Mtu mmoja katika umati akamjibu: “Mwalimu, nilimleta mwanangu kwako kwa sababu ana roho anayemfanya awe bubu.+ 18 Kila mara anapomshambulia humwangusha chini, naye hutoa povu mdomoni na kusaga meno yake na kuishiwa nguvu. Niliwaambia wanafunzi wako wamfukuze, lakini hawakuweza.” 19 Yesu akajibu: “Enyi kizazi kisicho na imani,+ nitaendelea kuwa pamoja nanyi mpaka lini? Nitawavumilia mpaka lini? Mleteni hapa.”+ 20 Basi wakamleta yule mvulana kwa Yesu, lakini yule roho mwovu alipomwona, mara moja akamfanya yule mtoto agaegae. Baada ya kuanguka chini, akaendelea kujiviringisha, akitoa povu mdomoni. 21 Yesu akamuuliza baba yake: “Jambo hili limekuwa likitokea kwa muda gani?” Akasema: “Tangu utotoni, 22 naye humwangusha ndani ya moto na ndani ya maji ili amuue. Lakini ikiwa unaweza kufanya chochote, tuhurumie na utusaidie.” 23 Yesu akamwambia: “Maneno hayo, ‘Ikiwa unaweza’! Mambo yote yanawezekana kwa mtu mwenye imani.”+ 24 Mara moja baba ya yule mtoto akasema kwa sauti kubwa: “Nina imani! Nisaidie mahali ambapo ninahitaji imani!”+
25 Yesu alipoona umati ukikusanyika haraka, akamkemea yule roho mwovu, akamwambia: “Wewe roho bubu na kiziwi, ninakuagiza umtoke mtoto huyu na usimwingie tena!”+ 26 Baada ya kupaza sauti na kugaagaa sana, roho huyo akamtoka, na yule mtoto akaonekana ni kama amekufa, hivi kwamba watu wengi wakasema: “Amekufa!” 27 Lakini Yesu akamshika mkono na kumwinua, naye akasimama. 28 Baada ya kuingia ndani ya nyumba, wanafunzi wake wakamuuliza faraghani: “Kwa nini tulishindwa kumfukuza?”+ 29 Akawaambia: “Roho wa aina hii hawezi kutoka isipokuwa kwa sala.”
30 Wakatoka huko wakapitia Galilaya, lakini hakutaka mtu yeyote ajue. 31 Kwa sababu alikuwa akiwafundisha wanafunzi wake na kuwaambia: “Mwana wa binadamu atasalitiwa mikononi mwa watu, nao watamuua,+ na ingawa atauawa, atafufuka baada ya siku tatu.”+ 32 Hata hivyo, hawakuelewa maneno aliyosema, nao waliogopa kumuuliza.
33 Nao wakaingia Kapernaumu. Alipokuwa ndani ya nyumba akawauliza: “Mlikuwa mkibishania nini barabarani?”+ 34 Wakakaa kimya, kwa maana barabarani walikuwa wakibishana kuhusu aliye mkuu kati yao. 35 Basi akaketi na kuwaita wale 12 akawaambia: “Yeyote anayetaka kuwa wa kwanza, lazima awe wa mwisho kati ya wote na mhudumu wa wote.”+ 36 Kisha akamchukua mtoto mdogo, akamsimamisha katikati yao; akamkumbatia na kuwaambia: 37 “Yeyote anayempokea mtoto mdogo+ kama huyu kwa msingi wa jina langu ananipokea mimi pia; na yeyote anayenipokea mimi hanipokei mimi tu, bali pia Yule aliyenituma.”+
38 Yohana akamwambia: “Mwalimu, tulimwona mtu fulani akifukuza roho waovu kwa kutumia jina lako, tukajaribu kumzuia, kwa sababu hakuwa akitufuata.”+ 39 Lakini Yesu akasema: “Msijaribu kumzuia, kwa maana hakuna yeyote atakayefanya matendo yenye nguvu kwa msingi wa jina langu atakayeweza kusema mambo mabaya kunihusu. 40 Kwa maana yeyote ambaye hatupingi yuko upande wetu.+ 41 Na yeyote anayewapa kikombe cha maji ya kunywa kwa sababu ninyi ni wa Kristo,+ kwa kweli ninawaambia hatapoteza kamwe thawabu yake.+ 42 Lakini yeyote anayemkwaza mmoja wa hawa wadogo walio na imani, ingekuwa afadhali ikiwa jiwe la kusagia ambalo huzungushwa na punda lingefungwa shingoni mwake kisha atupwe baharini.+
43 “Ikiwa mkono wako unakufanya ukwazike, ukate. Ni afadhali uingie katika uzima ukiwa kilema kuliko kuingia ukiwa na mikono miwili katika Gehena,* katika moto usioweza kuzimwa.+ 44* —— 45 Na ikiwa mguu wako unakufanya ukwazike, ukate. Ni afadhali uingie katika uzima ukiwa kilema kuliko kutupwa katika Gehena* ukiwa na miguu miwili.+ 46* —— 47 Na ikiwa jicho lako linakufanya ukwazike, litupe mbali.+ Ni afadhali uingie katika Ufalme wa Mungu ukiwa na jicho moja kuliko kutupwa katika Gehena ukiwa na macho mawili,*+ 48 mahali ambapo funza hawafi na moto hauzimwi.+
49 “Kwa maana kila mtu lazima atiwe chumvi kwa moto.+ 50 Chumvi ni nzuri, lakini ikipoteza ladha yake, mtaikoleza na nini?+ Iweni na chumvi ndani yenu,+ na mdumishe amani kati yenu.”+
10 Alipotoka hapo akaenda kwenye mipaka* ya Yudea, ng’ambo ya Yordani, na umati ukakusanyika tena karibu naye. Kama kawaida yake, akaanza tena kuwafundisha.+ 2 Mafarisayo wakaja, wakikusudia kumjaribu, wakamuuliza kama ni halali kwa mwanamume kumtaliki mke wake.+ 3 Akawajibu: “Musa aliwapa amri gani?” 4 Wakasema: “Musa aliruhusu kumwandikia cheti cha kumfukuza na kumtaliki.”+ 5 Lakini Yesu akawaambia: “Aliwaandikia amri hiyo+ kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu.+ 6 Hata hivyo, tangu mwanzo wa uumbaji ‘Aliwaumba mwanamume na mwanamke.+ 7 Kwa sababu hiyo, mwanamume atamwacha baba yake na mama yake,+ 8 na hao wawili watakuwa mwili mmoja,’+ basi wao si wawili tena, bali mwili mmoja. 9 Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha, mtu yeyote asikitenganishe.”+ 10 Walipoingia tena ndani ya nyumba wanafunzi wakaanza kumuuliza kuhusu jambo hilo. 11 Akawaambia: “Yeyote anayemtaliki mke wake na kumwoa mwingine anafanya uzinzi+ dhidi yake, 12 na ikiwa mwanamke baada ya kumtaliki mume wake anaolewa na mwingine, anafanya uzinzi.”+
13 Watu wakaanza kumletea watoto wadogo ili awaguse, lakini wanafunzi wakawakemea.+ 14 Alipoona hivyo, Yesu akakasirika na kuwaambia: “Waacheni watoto wadogo waje kwangu; msijaribu kuwazuia, kwa maana Ufalme wa Mungu ni wa wale walio kama hao.+ 15 Kwa kweli ninawaambia, yeyote asiyeupokea Ufalme wa Mungu kama mtoto mdogo hataingia kamwe ndani yake.”+ 16 Akawachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki, akiweka mikono yake juu yao.+
17 Alipokuwa akiondoka, mwanamume fulani akamkimbilia, akapiga magoti mbele yake na kumuuliza: “Mwalimu Mwema, ninapaswa kufanya nini ili niurithi uzima wa milele?”+ 18 Yesu akamwambia: “Kwa nini unaniita mwema? Hakuna aliye mwema, isipokuwa mmoja, Mungu.+ 19 Unazijua amri hizi: ‘Usiue,+ usifanye uzinzi,+ usiibe,+ usitoe ushahidi wa uwongo,+ usipunje,+ mheshimu baba yako na mama yako.’”+ 20 Mtu huyo akamwambia: “Mwalimu, nimeyashika mambo hayo yote tangu nilipokuwa kijana.” 21 Yesu akamtazama, akampenda na kumwambia: “Bado unahitaji kufanya jambo moja: Nenda ukauze vitu ulivyo navyo, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha uje uwe mfuasi wangu.”+ 22 Lakini akasikitishwa na jibu hilo, akaenda zake akiwa na huzuni, kwa maana alikuwa na mali nyingi.+
23 Yesu akatazama huku na huku na kuwaambia wanafunzi wake: “Itakuwa vigumu sana kwa wale walio na pesa kuingia katika Ufalme wa Mungu!”+ 24 Lakini wanafunzi wakashangazwa na maneno yake. Naye Yesu akawaambia: “Wanangu, ni vigumu sana kuingia katika Ufalme wa Mungu! 25 Ni rahisi zaidi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu.”+ 26 Wakazidi kushangaa wakamwambia:* “Ni nani anayeweza kuokolewa?”+ 27 Akawatazama moja kwa moja na kusema: “Kwa wanadamu haiwezekani, lakini sivyo ilivyo kwa Mungu, kwa maana mambo yote yanawezekana kwa Mungu.”+ 28 Petro akaanza kumwambia: “Tazama! Tumeacha kila kitu na kukufuata.”+ 29 Yesu akasema: “Kwa kweli ninawaambia, hakuna mtu aliyeacha nyumba au ndugu au dada au mama au baba au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema+ 30 ambaye hatapata mara 100 sasa katika kipindi hiki—nyumba, ndugu, dada, mama, watoto, mashamba, pamoja na mateso+—na katika mfumo wa mambo* unaokuja, uzima wa milele. 31 Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho, na wa mwisho watakuwa wa kwanza.”+
32 Sasa walikuwa barabarani wakipanda kwenda Yerusalemu, Yesu alikuwa akiwatangulia, nao walikuwa wameshangaa, lakini wale waliofuata wakaanza kuogopa. Akawapeleka kando tena wale 12 na kuanza kuwaambia mambo yaliyokuwa karibu kumpata:+ 33 “Tazama! Tunapanda kwenda Yerusalemu, na Mwana wa binadamu atatiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani na waandishi. Nao watamhukumia kifo na kumtia mikononi mwa watu wa mataifa, 34 nao watamdhihaki, watamtemea mate, watampiga mijeledi na kumuua, lakini baada ya siku tatu atafufuka.”+
35 Yakobo na Yohana, wana wa Zebedayo,+ wakaenda na kumwambia: “Mwalimu, tunataka utufanyie chochote tutakachokuomba.”+ 36 Akawauliza: “Mnataka niwafanyie nini?” 37 Wakamwambia: “Turuhusu tuketi, mmoja upande wako wa kuume na mwingine upande wako wa kushoto, katika utukufu wako.”+ 38 Lakini Yesu akawaambia: “Hamjui kile mnachoomba. Je, mnaweza kunywa kikombe ambacho ninakunywa au kubatizwa kwa ubatizo ninaobatizwa?”+ 39 Wakamwambia: “Tunaweza.” Ndipo Yesu akawaambia: “Kikombe ninachokunywa mtakunywa, na ubatizo ninaobatizwa mtabatizwa.+ 40 Hata hivyo, kuketi upande wangu wa kuume au wa kushoto sina haki ya kutoa, bali wataketi wale ambao wametayarishiwa.”
41 Wale wengine kumi waliposikia jambo hilo, wakawakasirikia Yakobo na Yohana.+ 42 Lakini Yesu akawaita akawaambia: “Mnajua kwamba wale wanaotawala* mataifa hupiga ubwana juu yao na wakuu wao hutumia mamlaka juu yao.+ 43 Haipaswi kuwa hivyo kati yenu; lakini yeyote anayetaka kuwa mkubwa kati yenu lazima awe mhudumu wenu,+ 44 na yeyote anayetaka kuwa wa kwanza kati yenu lazima awe mtumwa wa wote. 45 Kwa maana hata Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu+ na kutoa uhai wake uwe* fidia badala ya wengi.”+
46 Kisha wakafika Yeriko. Lakini yeye na wanafunzi wake na umati mkubwa walipokuwa wakitoka Yeriko, Bartimayo (mwana wa Timayo), kipofu aliyekuwa akiombaomba, alikuwa ameketi kando ya barabara.+ 47 Aliposikia kwamba ni Yesu Mnazareti, akaanza kusema kwa sauti kubwa: “Mwana wa Daudi,+ Yesu, nihurumie!”*+ 48 Ndipo wengi wakaanza kumkemea, wakimwambia anyamaze, lakini akazidi kusema kwa sauti kubwa: “Mwana wa Daudi, nihurumie!”* 49 Basi Yesu akasimama na kusema: “Mwiteni.” Nao wakamwita yule kipofu, wakamwambia: “Jipe moyo! Simama; anakuita.” 50 Akatupa vazi lake la nje, akasimama haraka na kumwendea Yesu. 51 Kisha Yesu akamwuliza: “Unataka nikufanyie nini?” Yule kipofu akamwambia: “Raboni,* naomba niweze kuona tena.” 52 Yesu akamwambia: “Nenda, imani yako imekuponya.”+ Na mara moja akaanza kuona,+ naye akaanza kumfuata barabarani.
11 Walipokuwa wakikaribia Yerusalemu, Bethfage na Bethania+ kwenye Mlima wa Mizeituni, akawatuma wawili kati ya wanafunzi wake,+ 2 akawaambia: “Nendeni katika kijiji mtakachokiona, na mara tu mtakapoingia mtamwona mwanapunda akiwa amefungwa, ambaye hakuna mtu amewahi kuketi juu yake. Mfungueni na kumleta. 3 Mtu yeyote akiwauliza, ‘Kwa nini mnamfungua?’ mwambieni, ‘Bwana anamhitaji, na atamrudisha hapa mara moja.’” 4 Basi wakaenda na kumpata mwanapunda akiwa amefungwa kwenye mlango, karibu na barabara, nao wakamfungua.+ 5 Lakini watu waliokuwa wamesimama hapo wakawauliza: “Kwa nini mnamfungua mwanapunda huyu?” 6 Wakajibu kama Yesu alivyowaambia, nao wakawaacha waende.
7 Wakampelekea Yesu huyo mwanapunda,+ wakatandika mavazi yao ya nje juu yake, naye akaketi juu yake.+ 8 Pia, wengi wakatandaza mavazi yao ya nje barabarani, lakini wengine wakatandaza matawi ya miti waliyokata katika mashamba.+ 9 Watu waliokuwa mbele na wale waliofuata nyuma wakaendelea kupaza sauti: “Tunaomba umwokoe!+ Amebarikiwa yule anayekuja katika jina la Yehova!*+ 10 Umebarikiwa Ufalme unaokuja wa baba yetu Daudi!+ Tunaomba umwokoe, katika vilele vilivyo juu!” 11 Akaingia Yerusalemu na kwenda hekaluni, akatazama vitu vyote huku na huku, lakini kwa kuwa muda ulikuwa umesonga sana, akaenda Bethania pamoja na wale 12.+
12 Siku iliyofuata, walipokuwa wakitoka Bethania, akahisi njaa.+ 13 Akaona kwa mbali mtini wenye majani, akaenda kuona kama angepata chochote. Lakini, alipoufikia, hakupata chochote ila majani, kwa maana hayakuwa majira ya tini. 14 Basi akauambia: “Mtu yeyote asile matunda yako tena kamwe.”+ Nao wanafunzi wake walikuwa wakisikiliza.
15 Wakafika Yerusalemu. Akaingia hekaluni akaanza kuwafukuza wale waliokuwa wakiuza na kununua hekaluni, naye akazipindua meza za wale waliokuwa wakibadili pesa na viti vya wale waliokuwa wakiuza njiwa,+ 16 na hakumruhusu mtu yeyote apite hekaluni akiwa amebeba chombo. 17 Alikuwa akiwafundisha akisema: “Je, haikuandikwa, ‘Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa ajili ya mataifa yote’?+ Lakini mmeifanya kuwa pango la wanyang’anyi.”+ 18 Wakuu wa makuhani na waandishi waliposikia hayo, wakaanza kutafuta njia ya kumuua;+ kwa maana walimwogopa, kwa sababu umati wote ulishangazwa na mafundisho yake.+
19 Ilipofika jioni, wakatoka jijini. 20 Lakini walipokuwa wakipita asubuhi na mapema, wakaona ule mtini ukiwa umenyauka kuanzia kwenye mizizi.+ 21 Petro, akaukumbuka na kumwambia: “Rabi, ona! ule mtini ulioulaani umenyauka.”+ 22 Yesu akawaambia: “Iweni na imani katika Mungu. 23 Kwa kweli ninawaambia mtu yeyote anayeuambia mlima huu, ‘Ng’oka, ukatupwe baharini,’ bila kuwa na shaka moyoni mwake lakini awe na imani kwamba yale anayosema yatatukia, itakuwa hivyo.+ 24 Ndiyo sababu ninawaambia, mambo yote mnayosali na kuomba, iweni na imani kwamba mmeyapokea, nanyi mtayapata.+ 25 Na mnaposimama kusali, wasameheni watu makosa waliyowatendea; ili Baba yenu aliye mbinguni awasamehe ninyi makosa yenu pia.”+ 26* ——
27 Wakaja tena Yerusalemu. Na alipokuwa akitembea hekaluni, wakuu wa makuhani, waandishi, na wazee wakaja 28 na kumuuliza: “Unafanya mambo haya kwa mamlaka gani? Au ni nani aliyekupa mamlaka ya kufanya mambo haya?”+ 29 Yesu akawaambia: “Nitawauliza swali moja. Mkinijibu, nitawaambia ninafanya mambo haya kwa mamlaka gani. 30 Je, ubatizo wa Yohana+ ulitoka mbinguni au kwa wanadamu?* Nijibuni.”+ 31 Basi wakaanza kujadiliana kati yao, wakisema: “Tukisema, ‘Ulitoka mbinguni,’ atatuuliza, ‘Basi, kwa nini hamkumwamini?’ 32 Lakini je, tutathubutu kusema, ‘Ulitoka kwa wanadamu’?” Kwa kuwa waliogopa umati, kwa maana umati wote uliamini kwa kweli Yohana alikuwa nabii.+ 33 Basi wakamjibu Yesu: “Hatujui.” Naye Yesu akawaambia: “Nami siwaambii ninafanya mambo haya kwa mamlaka gani.”
12 Akaanza kusema nao kwa mifano: “Mtu fulani alipanda shamba la mizabibu+ akalizungushia ua, akachimba shinikizo la divai, akajenga mnara,+ kisha akalikodisha kwa wakulima, naye akasafiri kwenda ng’ambo.+ 2 Majira yalipofika akamtuma mtumwa kwa wakulima ili achukue kutoka kwao baadhi ya matunda ya shamba la mizabibu. 3 Lakini wakamkamata, wakampiga na kumfukuza mikono mitupu. 4 Akamtuma tena mtumwa mwingine kwao, na huyo wakampiga kichwani na kumwaibisha.+ 5 Akamtuma mwingine, na huyo wakamuua, akawatuma wengine wengi, wakawapiga baadhi yao na kuwaua wengine. 6 Alikuwa na mmoja zaidi, mwana wake mpendwa.+ Mwishowe akamtuma kwao akisema: ‘Watamheshimu mwanangu.’ 7 Lakini wakulima wakaambiana, ‘Huyu ndiye mrithi.+ Njooni tumuue, na urithi utakuwa wetu.’ 8 Kwa hiyo wakamkamata, wakamuua na kumtupa nje ya shamba la mizabibu.+ 9 Mwenye shamba la mizabibu atafanya nini? Atakuja na kuwaua wakulima hao, kisha atawapa watu wengine shamba hilo la mizabibu.+ 10 Je, hamkusoma kamwe andiko hili: ‘Jiwe ambalo wajenzi walilikataa, limekuwa jiwe kuu la pembeni.*+ 11 Hili limetoka kwa Yehova,* na ni lenye kustaajabisha machoni petu’?”+
12 Ndipo wakataka kumkamata, lakini waliuogopa umati, kwa maana walijua kwamba mfano aliosema uliwahusu. Basi wakamwacha na kwenda zao.+
13 Kisha wakawatuma baadhi ya Mafarisayo na wafuasi wa chama cha Herode ili wamnase kwa maneno yake.+ 14 Walipofika wakamwambia: “Mwalimu, tunajua wewe husema ukweli na hutafuti kibali cha yeyote, kwa maana huangalii sura ya nje ya mtu, bali unafundisha njia ya Mungu kupatana na kweli. Je, ni halali* au si halali kumlipa Kaisari kodi?* 15 Je, tunapaswa kulipa, au hatupaswi kulipa?” Akagundua unafiki wao, akawaambia: “Kwa nini mnanijaribu? Nileteeni dinari* niitazame.” 16 Wakaleta dinari moja, akawauliza: “Sura hii na maandishi haya ni ya nani?” Wakajibu: “Ni ya Kaisari.” 17 Ndipo Yesu akasema: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari,+ na Mungu vitu vya Mungu.”+ Nao wakashangazwa naye.
18 Sasa Masadukayo, ambao husema hakuna ufufuo,+ wakaja na kumuuliza:+ 19 “Mwalimu, Musa alituandikia kwamba mtu akifa na kuacha mke lakini hakuacha mtoto, ndugu yake anapaswa kumchukua mke huyo ili kumwinulia ndugu yake uzao.+ 20 Kulikuwa na ndugu saba. Wa kwanza alioa mwanamke, lakini alipokufa hakuacha uzao wowote. 21 Wa pili akamwoa, lakini akafa bila kuacha uzao, na wa tatu vivyo hivyo. 22 Na wote saba hawakuacha uzao. Mwishowe pia yule mwanamke akafa. 23 Katika ufufuo atakuwa mke wa nani? Kwa maana wote saba walikuwa wamemwoa.” 24 Yesu akawaambia: “Ninyi mmekosea kwa sababu hamjui Maandiko wala nguvu za Mungu.+ 25 Kwa maana wanapofufuliwa kutoka kwa wafu, wanaume hawaoi wala wanawake hawaolewi, bali wao ni kama malaika mbinguni.+ 26 Lakini kuhusu kufufuliwa kwa wafu, je, hamkusoma katika kitabu cha Musa, simulizi kuhusu kile kichaka cha miiba kwamba Mungu alimwambia: ‘Mimi ni Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo’?+ 27 Yeye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai. Mmekosea sana.”+
28 Mmoja kati ya waandishi waliokuwa wamekuja na kusikia wakibishana, akijua kwamba alikuwa amewajibu vizuri, akamuuliza: “Ni amri gani iliyo ya kwanza* kati ya zote?”+ 29 Yesu akajibu: “Ya kwanza ni hii, ‘Sikilizeni, enyi Waisraeli, Yehova* Mungu wetu ni Yehova* mmoja, 30 nawe lazima umpende Yehova* Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi* yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.’+ 31 Ya pili ni hii, ‘Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.’+ Hakuna amri nyingine iliyo kubwa kuliko amri hizi.” 32 Yule mwandishi akamwambia: “Mwalimu, umesema vema kupatana na kweli, ‘Yeye ni Mmoja, na hakuna mwingine isipokuwa yeye’;+ 33 na kumpenda Mungu kwa moyo wote na kwa uelewaji wote na kwa nguvu zote na pia mtu kumpenda jirani yake kama anavyojipenda mwenyewe ni bora kuliko matoleo yote mazima ya kuteketezwa na dhabihu.”+ 34 Yesu alipotambua kwamba amejibu kwa kutumia akili, akamwambia: “Wewe huko mbali na Ufalme wa Mungu.” Lakini hakuna mtu aliyethubutu tena kumuuliza swali.+
35 Hata hivyo, Yesu akiendelea kufundisha hekaluni, akawauliza: “Kwa nini waandishi husema kwamba Kristo ni mwana wa Daudi?+ 36 Kupitia roho takatifu+ Daudi mwenyewe alisema, ‘Yehova* alimwambia Bwana wangu: “Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwaweke maadui wako chini ya miguu yako.”’+ 37 Daudi mwenyewe anamwita Bwana, basi Kristo anawezaje kuwa mwanawe?”+
Na umati mkubwa ulikuwa ukimsikiliza kwa furaha. 38 Akaendelea kufundisha akisema: “Jihadharini na waandishi kwa kuwa wanapenda kutembea wakiwa wamevaa kanzu na wanapenda kusalimiwa sokoni+ 39 na viti vya mbele* katika masinagogi na mahali penye heshima zaidi kwenye milo ya jioni.+ 40 Wao ndio wanaomaliza nyumba* za wajane na kutoa sala ndefu ili waonekane.* Hao watapata hukumu kali zaidi.”*
41 Kisha akaketi akitazama masanduku* ya hazina+ na kuanza kuangalia jinsi umati ulivyokuwa ukitumbukiza pesa katika masanduku hayo, na matajiri wengi walikuwa wakitumbukiza sarafu nyingi.+ 42 Mjane fulani maskini akaja akatumbukiza sarafu mbili ndogo zenye thamani ndogo sana.*+ 43 Basi akawaita wanafunzi wake na kuwaambia: “Kwa kweli ninawaambia mjane huyu maskini ametumbukiza zaidi ya wote waliotumbukiza pesa ndani ya masanduku ya hazina.+ 44 Kwa maana wote walitumbukiza kutokana na ziada yao, lakini yeye, ingawa ni maskini,* alitumbukiza kila kitu alichokuwa nacho, riziki yake yote.”+
13 Alipokuwa akitoka hekaluni mmoja wa wanafunzi wake akamwambia: “Mwalimu, ona! jinsi mawe na majengo haya yalivyo maridadi!”+ 2 Hata hivyo, Yesu akamwambia: “Unayaona majengo haya makubwa? Hakuna jiwe litakaloachwa hapa juu ya jiwe lingine bila kuangushwa chini.”+
3 Alipokuwa ameketi kwenye Mlima wa Mizeituni, huku hekalu likiwa linaonekana, Petro, Yakobo, Yohana, na Andrea wakamuuliza faraghani: 4 “Tuambie, mambo haya yatatukia lini, na nini itakayokuwa ishara ya wakati ambapo mambo haya yatafikia mwisho?”+ 5 Basi Yesu akaanza kuwaambia: “Jihadharini ili mtu yeyote asiwapotoshe.+ 6 Wengi watakuja kwa msingi wa jina langu, wakisema, ‘Mimi ndiye,’ nao watawapotosha wengi. 7 Zaidi ya hayo, mtakaposikia kuhusu vita na habari za vita, msiogope; lazima mambo hayo yatukie, lakini ule mwisho bado.+
8 “Kwa maana taifa litapigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme;+ kutakuwa na matetemeko ya ardhi sehemu mbalimbali; pia kutakuwa na upungufu wa chakula.+ Mambo hayo ni mwanzo wa maumivu ya taabu.+
9 “Lakini ninyi jihadharini. Watu watawapeleka mahakamani,+ nanyi mtapigwa katika masinagogi+ na kusimamishwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu, ili kuwa ushahidi kwao.+ 10 Pia, katika mataifa yote, lazima habari njema ihubiriwe kwanza.+ 11 Na watakapokuwa wakiwapeleka kuwashtaki, msihangaike kuhusu jambo mtakalosema; bali semeni jambo mtakalopewa saa hiyo, kwa maana si ninyi mnaosema, bali ni roho takatifu.+ 12 Isitoshe, ndugu atamtoa ndugu yake ili auawe, na baba atamtoa mtoto, na watoto watainuka dhidi ya wazazi na kufanya wauawe.+ 13 Nanyi mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu.+ Lakini yule atakayevumilia* mpaka mwisho+ ndiye atakayeokolewa.+
14 “Hata hivyo, mtakapoona kile kitu chenye kuchukiza sana kinachosababisha ukiwa+ kikiwa kimesimama mahali ambapo hakipaswi kuwa (msomaji na atumie utambuzi), ndipo wale walio Yudea waanze kukimbilia milimani.+ 15 Mtu aliye juu ya paa la nyumba asishuke wala asiingie kuchukua kitu chochote ndani ya nyumba yake; 16 na mtu aliye shambani asirudi kwenye vitu vilivyo nyuma ili kuchukua vazi lake la nje. 17 Ole wao wanawake wenye mimba na wale wanaonyonyesha mtoto katika siku hizo!+ 18 Endeleeni kusali kwamba isitukie wakati wa majira ya baridi kali; 19 kwa maana siku hizo zitakuwa za dhiki+ ambayo haijawahi kutokea tangu mwanzo wa uumbaji ambao Mungu aliumba mpaka wakati huo, na haitatokea tena.+ 20 Kwa kweli, kama Yehova* hangezifupisha siku hizo, hakuna mwili wowote ambao ungeokolewa. Lakini kwa sababu ya wale waliochaguliwa ambao amewachagua, amezifupisha siku hizo.+
21 “Pia, mtu yeyote akiwaambia, ‘Tazama! Kristo yuko hapa,’ ‘Tazama! yuko pale,’ msiamini.+ 22 Kwa maana Kristo wengi wa uwongo na manabii wa uwongo+ watatokea na kufanya ishara na maajabu ili kuwapotosha, ikiwezekana, hata wale waliochaguliwa. 23 Basi, jihadharini.+ Nimewaambia mambo yote mapema.
24 “Lakini katika siku hizo, baada ya dhiki hiyo, jua litatiwa giza, na mwezi hautatoa nuru yake,+ 25 nazo nyota zitakuwa zikianguka kutoka mbinguni na nguvu zilizo katika mbingu zitatikiswa. 26 Ndipo watakapomwona Mwana wa binadamu+ akija katika mawingu akiwa na nguvu nyingi na utukufu.+ 27 Kisha atawatuma malaika wawakusanye watu wake waliochaguliwa kutoka kwenye zile pepo nne, kuanzia mwisho wa dunia mpaka mwisho wa mbingu.+
28 “Basi jifunzeni mfano huu kutokana na mtini: Mara tu matawi yake machanga yanapokuwa laini na kuchipua majani, mnajua kwamba kiangazi kinakaribia.+ 29 Vivyo hivyo, ninyi pia mtakapoona mambo hayo yakitukia, jueni kwamba yuko karibu, yuko mlangoni.+ 30 Kwa kweli ninawaambia kizazi hiki hakitapitilia mbali kamwe mpaka mambo haya yote yatukie.+ 31 Mbingu na dunia zitapitilia mbali,+ lakini maneno yangu hayatapitilia mbali kamwe.+
32 “Kuhusu siku hiyo au saa hiyo hakuna mtu anayejua, wala malaika mbinguni wala Mwana, ila Baba.+ 33 Endeleeni kutazama, endeleeni kukaa macho,+ kwa maana hamjui wakati uliowekwa ni lini.+ 34 Ni kama mtu anayesafiri ng’ambo ambaye aliacha nyumba yake na kuwapa watumwa wake mamlaka,+ kila mmoja kazi yake, na kumwamuru mlinzi wa mlango aendelee kukesha.+ 35 Kwa hiyo, endeleeni kukesha, kwa maana hamjui bwana wa nyumba anakuja wakati gani,+ iwe ni jioni, usiku wa manane, kabla ya alfajiri,* au asubuhi na mapema,+ 36 ili anapofika ghafla, asiwakute mkiwa mmelala usingizi.+ 37 Lakini ninachowaambia ninyi, ninawaambia pia watu wote: Endeleeni kukesha.”+
14 Sasa ilikuwa siku mbili kabla+ ya Pasaka+ na Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu.+ Nao wakuu wa makuhani na waandishi walikuwa wakitafuta njia ya kumkamata Yesu kwa hila* na kumuua;+ 2 kwa maana walikuwa wakisema: “Si kwenye sherehe; huenda watu wakafanya ghasia.”
3 Alipokuwa Bethania akila* katika nyumba ya Simoni mwenye ukoma, mwanamke fulani akaja na chupa ya alabasta iliyokuwa na mafuta yenye marashi, nardo halisi, ghali sana. Akaifungua na kuanza kuyamimina juu ya kichwa cha Yesu.+ 4 Ndipo baadhi yao wakakasirika na kuambiana: “Kwa nini mafuta haya ya marashi yapotezwe bure? 5 Kwa maana mafuta haya yangeuzwa kwa zaidi ya dinari* 300 na maskini wapewe pesa hizo!” Nao wakamkasirikia* sana mwanamke huyo. 6 Lakini Yesu akawaambia: “Mwacheni. Kwa nini mnataka kumsumbua? Amenitendea jambo jema.+ 7 Kwa maana maskini mnao sikuzote,+ na mnaweza kuwasaidia wakati wowote mnaotaka, lakini mimi hamtakuwa nami sikuzote.+ 8 Amefanya alichoweza; ameupaka mwili wangu mafuta yenye marashi ili kuutayarisha kwa ajili ya mazishi.+ 9 Kwa kweli ninawaambia, popote ambapo habari njema itahubiriwa ulimwenguni,+ jambo alilofanya mwanamke huyu litatajwa ili kumkumbuka.”+
10 Yuda Iskariote, mmoja wa wale 12, akaenda kwa wakuu wa makuhani ili amsaliti kwao.+ 11 Waliposikia hilo, wakafurahi na kuahidi kumpa fedha.+ Basi akaanza kutafuta nafasi ya kumsaliti.
12 Sasa siku ya kwanza ya Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu,+ wakati ambapo walikuwa na desturi ya kutoa dhabihu ya Pasaka,+ wanafunzi wake wakamwuliza: “Unataka twende tukutayarishie wapi mlo wa Pasaka?”+ 13 Ndipo akawatuma wawili kati ya wanafunzi wake akawaambia: “Nendeni jijini, nanyi mtakutana na mwanamume akiwa amebeba mtungi wa maji. Mfuateni,+ 14 na popote atakapoingia, mwambieni mwenye nyumba, ‘Mwalimu anasema: “Kiko wapi chumba cha wageni ambamo ninaweza kula Pasaka pamoja na wanafunzi wangu?”’ 15 Naye atawaonyesha chumba kikubwa cha juu, chenye vifaa na kilichotayarishwa. Tuandalieni humo.” 16 Basi wanafunzi wakaenda, wakaingia jijini na kupata kama alivyowaambia, nao wakaandaa Pasaka.
17 Ilipofika jioni akaja pamoja na wale 12.+ 18 Walipokuwa wameketi mezani wakila, Yesu akasema: “Kwa kweli ninawaambia, mmoja wenu anayekula pamoja nami atanisaliti.”+ 19 Wakaanza kuhuzunika na kumuuliza mmoja baada ya mwingine: “Je, ni mimi?” 20 Akawaambia: “Ni mmoja kati yenu 12, anayechovya pamoja nami katika bakuli.+ 21 Kwa maana Mwana wa binadamu anaenda zake, kama ilivyoandikwa kumhusu, lakini ole wake mtu atakayemsaliti Mwana wa binadamu!+ Ingekuwa afadhali kama mtu huyo hangezaliwa.”+
22 Walipokuwa wakiendelea kula, akachukua mkate, akatoa baraka, akaumega, akawapa, na kusema: “Chukueni; huu unamaanisha mwili wangu.”+ 23 Kisha akachukua kikombe, akashukuru na kuwapa, wote wakanywa kutoka kwenye kikombe hicho.+ 24 Akawaambia: “Hii inamaanisha ‘damu+ yangu ya agano,’+ ambayo itamwagwa kwa ajili ya wengi.+ 25 Kwa kweli ninawaambia, sitakunywa tena kamwe divai ya mzabibu mpaka siku nitakapokunywa ikiwa mpya katika Ufalme wa Mungu.” 26 Mwishowe, baada ya kuimba sifa,* wakaenda kwenye Mlima wa Mizeituni.+
27 Yesu akawaambia: “Ninyi nyote mtakwazika, kwa maana imeandikwa: ‘Nitampiga mchungaji,+ nao kondoo watatawanyika.’+ 28 Lakini baada ya kufufuliwa, nitawatangulia kuingia Galilaya.”+ 29 Lakini Petro akamwambia: “Hata wengine wote wakikwazika, mimi sitakwazika.”+ 30 Ndipo Yesu akamwambia: “Kwa kweli ninakuambia kwamba leo, ndiyo, usiku huu, kabla jogoo hajawika mara mbili, utanikana mara tatu.”+ 31 Lakini akaendelea kusisitiza: “Hata nikilazimika kufa pamoja nawe, sitakukana kamwe.” Pia, wengine wote wakaanza kusema vivyo hivyo.+
32 Basi wakafika mahali panapoitwa Gethsemane, akawaambia wanafunzi wake: “Ketini hapa ninaposali.”+ 33 Akaondoka pamoja na Petro, Yakobo, na Yohana,+ naye akaanza kufadhaika* na kutaabika sana. 34 Akawaambia: “Nimehuzunika* sana,+ kiasi cha kufa. Kaeni hapa na mwendelee kukesha.”+ 35 Akasonga mbele kidogo, akaanguka chini na kuanza kusali kwamba ikiwezekana, saa hiyo ipitilie mbali kutoka kwake. 36 Naye akasema: “Abba,* Baba,+ mambo yote yanawezekana kwako; niondolee kikombe hiki. Lakini si kama ninavyotaka, bali unavyotaka.”+ 37 Aliporudi akawakuta wakiwa wamelala usingizi, akamwuliza Petro: “Simoni, unalala? Hukuwa na nguvu za kukesha hata kwa saa moja?+ 38 Endeleeni kukesha na kusali bila kuacha, ili msiingie katika majaribu.+ Bila shaka, roho inataka,* lakini mwili ni dhaifu.”+ 39 Naye akaenda zake tena, akasali, akirudia maneno yaleyale.+ 40 Akaja tena na kuwakuta wakiwa wamelala usingizi, kwa maana macho yao yalikuwa yamelemewa, nao hawakujua la kumjibu. 41 Akarudi mara ya tatu akawaambia: “Mnalala na kupumzika wakati kama huu! Imetosha! Saa imefika!+ Tazama! Mwana wa binadamu anasalitiwa mikononi mwa watenda dhambi. 42 Simameni twende. Tazama! Msaliti wangu amekaribia.”+
43 Na mara moja, alipokuwa bado akizungumza, Yuda, mmoja wa wale 12, akafika pamoja na umati wenye mapanga na marungu, walikuwa wametumwa na wakuu wa makuhani, waandishi, na wazee.+ 44 Basi msaliti wake alikuwa amewapa ishara waliyokubaliana akisema: “Yule nitakayembusu, huyo ndiye; mkamateni na kuondoka naye akiwa chini ya ulinzi.” 45 Akaja moja kwa moja akamkaribia na kusema, “Rabi!” kisha akambusu kwa wororo. 46 Basi wakamkamata na kumtia nguvuni. 47 Hata hivyo, mmoja wa wale waliokuwa wamesimama hapo akauchomoa upanga wake, akampiga mtumwa wa kuhani mkuu na kumkata sikio.+ 48 Lakini Yesu akawaambia: “Je, mmekuja kunikamata mkiwa na mapanga na marungu kana kwamba mimi ni mwizi?+ 49 Siku baada ya siku nilikuwa nanyi nikifundisha hekaluni,+ lakini hamkunikamata. Hata hivyo, ni ili Maandiko yatimizwe.”+
50 Ndipo wote wakamwacha na kukimbia.+ 51 Hata hivyo, kijana fulani aliyevaa vazi la kitani bora juu ya mwili wake ulio uchi akaanza kumfuata kwa karibu, nao wakajaribu kumkamata, 52 lakini akaliacha vazi lake la kitani, akakimbia akiwa uchi.*
53 Kisha wakampeleka Yesu kwa kuhani mkuu,+ nao wakuu wote wa makuhani, wazee, na waandishi wakakusanyika.+ 54 Lakini Petro akamfuata kwa mbali mpaka kwenye ua wa kuhani mkuu; akaketi pamoja na watumishi wa nyumbani akiota moto mwangavu.+ 55 Sasa wakuu wa makuhani na Sanhedrini yote walikuwa wakitafuta ushahidi dhidi ya Yesu ili wamuue, lakini hawakupata.+ 56 Kwa kweli, wengi walikuwa wakitoa ushahidi wa uwongo kumhusu,+ lakini ushahidi wao haukupatana. 57 Pia, wengine walikuwa wakisimama na kutoa ushahidi wa uwongo kumhusu, wakisema: 58 “Tulimsikia akisema, ‘Nitaliangusha chini hekalu hili lililojengwa kwa mikono, na kwa siku tatu nitajenga lingine ambalo halijajengwa kwa mikono.’”+ 59 Lakini hata kwa misingi hiyo, ushahidi wao haukupatana.
60 Kisha kuhani mkuu akasimama katikati yao, akamuuliza Yesu: “Kwa nini hujibu? Watu hawa wanashuhudia nini kukuhusu?”+ 61 Lakini akakaa kimya na hakujibu.+ Tena kuhani mkuu akaanza kumuuliza: “Je, wewe ndiye Kristo Mwana wa Yule Mbarikiwa?” 62 Ndipo Yesu akasema: “Mimi ndiye; nanyi mtamwona Mwana wa binadamu+ akiwa ameketi kwenye mkono wa kuume+ wa nguvu, akija pamoja na mawingu ya mbinguni.”+ 63 Ndipo kuhani mkuu akayararua mavazi yake na kusema: “Tunahitaji mashahidi wengine wa nini?+ 64 Mmemsikia akikufuru. Uamuzi wenu ni nini?”* Wote wakaamua kwamba anastahili kufa.+ 65 Wengine wakaanza kumtemea mate,+ wakamfunika uso, wakampiga ngumi na kumwambia: “Toa unabii!” Walinzi wa mahakama wakampiga makofi usoni na kumchukua.+
66 Sasa Petro alipokuwa chini katika ua, mmoja wa wajakazi wa kuhani mkuu akaja.+ 67 Alipomwona Petro akiota moto, akamtazama moja kwa moja na kusema: “Hata wewe ulikuwa pamoja na Yesu Mnazareti.” 68 Lakini akakana, akisema: “Simjui wala sielewi unachosema.” Kisha akatoka na kuelekea langoni.* 69 Yule kijakazi alipomwona akaanza tena kuwaambia wale waliosimama hapo: “Huyu ni mmoja wao.” 70 Petro akakana tena. Baada ya muda mfupi, wale waliosimama hapo wakaanza tena kumwambia: “Hakika wewe ni mmoja wao, kwa maana, wewe ni Mgalilaya.” 71 Lakini akaanza kulaani na kuapa: “Simjui mtu huyu mnayezungumza kumhusu!” 72 Papo hapo jogoo akawika mara ya pili,+ naye Petro akakumbuka maneno ambayo Yesu alimwambia: “Kabla jogoo hajawika mara mbili, utanikana mara tatu.”+ Naye akalemewa akaanza kulia.
15 Mara tu kulipopambazuka wakuu wa makuhani, wazee, na waandishi, yaani, Sanhedrini yote, wakashauriana pamoja na kumfunga Yesu, kisha wakampeleka na kumkabidhi kwa Pilato.+ 2 Basi Pilato akamuuliza: “Je, wewe ndiye Mfalme wa Wayahudi?”+ Akamjibu: “Wewe mwenyewe umesema.”+ 3 Lakini wakuu wa makuhani walikuwa wakimshtaki kwa mambo mengi. 4 Pilato akaanza kumuuliza tena: “Je, huna jibu lolote?+ Ona ni mashtaka mangapi wanayoleta dhidi yako.”+ 5 Lakini Yesu hakujibu tena, hivi kwamba Pilato akashangaa.+
6 Basi, kila sherehe ya Pasaka, alikuwa na desturi ya kuwafungulia mfungwa ambaye waliomba.+ 7 Wakati huo mtu aliyeitwa Baraba alikuwa amefungwa pamoja na wachochezi ambao katika uchochezi wao walikuwa wameua. 8 Basi umati ukaja na kuanza kumwomba Pilato awafanyie kama ilivyokuwa desturi yake. 9 Akawauliza: “Je, mnataka niwafungulie Mfalme wa Wayahudi?”+ 10 Kwa maana Pilato alijua kwamba wakuu wa makuhani walikuwa wamemkabidhi Yesu kwake kwa sababu ya wivu.+ 11 Lakini wakuu wa makuhani wakauchochea umati umwombe awafungulie Baraba badala yake.+ 12 Pilato akawauliza tena: “Basi, nifanye nini na mtu huyu mnayemwita Mfalme wa Wayahudi?”+ 13 Kwa mara nyingine tena wakapaza sauti: “Atundikwe mtini!”*+ 14 Lakini Pilato akawaambia: “Kwa nini? Amefanya kosa gani?” Hata hivyo, wakaendelea kupaza sauti hata zaidi: “Atundikwe mtini!”*+ 15 Basi Pilato akitaka kuuridhisha umati, akawafungulia Baraba; akaagiza Yesu apigwe mijeledi,+ kisha akamtoa ili auawe kwenye mti.+
16 Sasa wanajeshi wakampeleka kwenye ua, katika makao ya gavana, nao wakakusanya kikosi chote cha wanajeshi.+ 17 Wakamvika Yesu vazi la zambarau, wakasokota taji la miiba na kumvisha; 18 nao wakaanza kumwambia kwa sauti kubwa: “Salamu,* ewe Mfalme wa Wayahudi!”+ 19 Pia, walikuwa wakimpiga kichwani kwa utete na kumtemea mate, nao wakapiga magoti na kumsujudia.* 20 Mwishowe, baada ya kumdhihaki, wakamvua lile vazi la zambarau na kumvisha mavazi yake ya nje. Kisha wakampeleka ili kumtundika mtini.+ 21 Pia, wakamlazimisha mpita njia afanye utumishi, mtu fulani aitwaye Simoni wa Kirene, baba ya Aleksanda na Rufo, aliyekuwa akitoka mashambani, aubebe mti wa mateso* wa Yesu.+
22 Basi wakampeleka mahali panapoitwa Golgotha, neno ambalo linapotafsiriwa linamaanisha, “Mahali pa Fuvu la Kichwa.”+ 23 Hapa wakajaribu kumpa divai iliyotiwa kileo cha manemane,+ lakini hakuinywa. 24 Nao wakamtundika kwenye mti na wakagawana mavazi yake kwa kuyapigia kura ili kuamua ni nini ambacho kila mtu angechukua.+ 25 Ilikuwa saa tatu,* nao wakamtundika kwenye mti. 26 Na maandishi ya mashtaka dhidi yake yalikuwa yameandikwa: “Mfalme wa Wayahudi.”+ 27 Pia, wakawatundika wezi wawili kwenye mti kando yake, mmoja upande wake wa kuume na mwingine upande wake wa kushoto.+ 28* —— 29 Wale waliokuwa wakipita hapo wakamtukana huku wakitikisa vichwa vyao+ wakisema: “Aha! Wewe uliyetaka kuliangusha chini hekalu na kulijenga kwa siku tatu,+ 30 jiokoe mwenyewe kwa kushuka kutoka kwenye mti wa mateso.”* 31 Vivyo hivyo, wakuu wa makuhani na waandishi walikuwa wakimdhihaki kati yao wakisema: “Aliwaokoa wengine lakini hawezi kujiokoa mwenyewe!+ 32 Acheni Kristo, Mfalme wa Israeli, ashuke sasa kutoka kwenye mti wa mateso,* ili tuone na kuamini.”+ Hata wale waliotundikwa mtini kando yake walikuwa wakimshutumu.+
33 Ilipofika saa sita* kukawa na giza katika nchi yote mpaka saa tisa.*+ 34 Na saa tisa Yesu akapaza sauti: “Eli, Eli, lama sabakthani?” maneno hayo yanapotafsiriwa yanamaanisha, “Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?”+ 35 Na baadhi ya wale waliokuwa wamesimama karibu walipomsikia wakaanza kusema: “Sikia! Anamwita Eliya.” 36 Kisha mtu fulani akakimbia, akalowesha sifongo katika divai kali, akaiweka kwenye utete, akampa anywe,+ akisema: “Mwacheni! Acheni tuone kama Eliya atakuja kumshusha.” 37 Lakini Yesu akalia kwa sauti kubwa, akakata pumzi.*+ 38 Na pazia la patakatifu+ likapasuka vipande viwili kuanzia juu mpaka chini.+ 39 Sasa ofisa wa jeshi aliyekuwa amesimama kando yake akimtazama, alipoona amekufa katika hali hizo, akasema: “Hakika mtu huyu alikuwa Mwana wa Mungu.”+
40 Kulikuwa pia na wanawake wakitazama kwa mbali, miongoni mwao kulikuwa na Maria Magdalene, Salome, na Maria mama ya Yakobo Mdogo na Yose,+ 41 walikuwa wakifuatana na Yesu na kumhudumia+ alipokuwa Galilaya, pia wanawake wengine wengi waliokuwa wamekuja Yerusalemu pamoja naye.
42 Sasa kwa kuwa ilikuwa jioni, siku ya Matayarisho, yaani, siku moja kabla ya Sabato, 43 akaja Yosefu wa Arimathea, mshiriki wa Baraza aliyeheshimiwa, ambaye pia alikuwa akiungojea Ufalme wa Mungu. Akajipa moyo na kwenda kwa Pilato, akaomba apewe mwili wa Yesu.+ 44 Lakini Pilato akataka kujua kama tayari alikuwa amekufa, akamwita yule ofisa wa jeshi, akamuuliza ikiwa Yesu alikuwa amekufa. 45 Baada ya kuhakikisha kutoka kwa huyo ofisa wa jeshi, akamruhusu Yosefu auchukue mwili huo. 46 Baada ya kununua kitani bora, akamshusha na kumfunga kwa kile kitani bora na kumlaza katika kaburi*+ lililokuwa limechimbwa katika mwamba; kisha akaviringisha jiwe kwenye mwingilio wa lile kaburi.+ 47 Lakini Maria Magdalene na Maria mama ya Yose wakaendelea kutazama mahali alipokuwa amelazwa.+
16 Baada ya Sabato+ kupita, Maria Magdalene, Maria+ mama ya Yakobo, na Salome wakanunua manukato ili wakaupake mwili wa Yesu.+ 2 Asubuhi na mapema siku ya kwanza ya juma, jua lilipokuwa limechomoza, wakaenda kwenye kaburi.*+ 3 Walikuwa wakiulizana: “Ni nani atakayetuviringishia lile jiwe kutoka kwenye mwingilio wa kaburi?” 4 Lakini walipotazama, wakaona lile jiwe lilikuwa limeondolewa, ingawa lilikuwa kubwa sana.+ 5 Walipoingia ndani ya kaburi, wakaona mwanamume kijana akiwa ameketi upande wa kulia akiwa amevaa kanzu nyeupe, nao wakashtuka. 6 Akawaambia: “Msishtuke.+ Mnamtafuta Yesu Mnazareti, aliyeuawa kwenye mti. Amefufuliwa.+ Hayupo hapa. Tazama, hapa ndipo walipomlaza.+ 7 Lakini nendeni mkawaambie wanafunzi wake na Petro, ‘Yesu anawatangulia kwenda Galilaya.+ Mtamwona huko, kama vile alivyowaambia.’”+ 8 Basi walipotoka kaburini, wakakimbia wakitetemeka huku wakiwa wamelemewa na hisia. Nao hawakumwambia mtu yeyote jambo lolote, kwa sababu waliogopa.*+
Tnn., “mbele ya uso wako.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “akawatumbukiza; akawazamisha.”
Au labda, “walijua yeye ni nani.”
Au “machela.”
Au “alipokuwa ameketi mezani.”
Au “walikuwa wameketi mezani.”
Au “mikate iliyowekwa mbele za Mungu.”
Au “nafsi.”
Au “Akachagua.”
Au “alichochagua.”
Au “mwenye bidii.”
Jina lingine la Shetani.
Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Au “kikapu cha kupimia.”
Au “kwa nini mna hofu?”
Au “makaburi ya ukumbusho.”
Au “ukingo wenye mteremko mkali.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “Eneo lenye Majiji Kumi.”
Au “akapiga magoti mbele yake.”
Au “anakaribia kufa.”
Au “alikuwa ameumizwa sana.”
Au “onyesha tu imani.”
Au “akawaamuru kwa uthabiti.”
Tnn., “shaba.”
Au “vazi la ziada.”
Au “wale waliokuwa wameketi mezani.”
Au “wale waliokuwa wameketi mezani.”
Au “katika kaburi la ukumbusho.”
Angalia Nyongeza B14.
Yaani, karibu saa 9 usiku hadi karibu saa 12 asubuhi.
Au “alikuwa karibu.”
Au “machela.”
Yaani, haikuwa imesafishwa kisherehe.
Au “kuzamisha.”
Au “Anayesema vibaya kumhusu.”
Angalia Nyongeza A3.
Wingi wa neno la Kigiriki, por·neiʹa. Angalia Kamusi.
Au “ufidhuli; matendo ya kuchukiza yanayofanywa bila aibu.” Kigiriki, a·selʹgei·a. Angalia Kamusi.
Au “aliyezaliwa huko.”
Au “Eneo lenye Majiji Kumi.”
Au “wakiwa wamefunga.”
Au “hamira.”
Angalia Kamusi, “Mti wa mateso.”
Au “nafsi yake ataipoteza.”
Au “nafsi yake.”
Au “nafsi yake.”
Au “nafsi yake.”
Au “kisicho na uaminifu.”
Au labda, “hawakumwambia mtu yeyote.”
Angalia Kamusi.
Angalia Nyongeza A3.
Angalia Kamusi.
Angalia Nyongeza A3.
Angalia Kamusi.
Au “karibu na mipaka.”
Au labda, “wakaambiana.”
Angalia Kamusi.
Au “wanaoonwa kuwa watawala wa.”
Au “nafsi yake iwe.”
Au “nionyeshe rehema!”
Au “nionyeshe rehema!”
Maana yake “Mwalimu.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A3.
Au “chanzo chake ni wanadamu?”
Tnn., “kichwa cha pembeni.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “ni sawa.”
Au “kodi ya kichwa.”
Angalia Nyongeza B14.
Au “muhimu zaidi.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Kamusi.
Angalia Nyongeza A5.
Au “mahali bora.”
Au “mali.”
Au “kujifanya.”
Au “watapokea hukumu nzito.”
Au “makasha.”
Tnn., “leptoni mbili, ambazo ni kwadrani moja.” Angalia Nyongeza B14.
Au “ana uhitaji.”
Au “anayevumilia.”
Angalia Nyongeza A5.
Tnn., “jogoo anapowika.”
Au “kwa ujanja.”
Au “akiwa ameketi mezani.”
Angalia Nyongeza B14.
Au “wakamkemea.”
Au “zaburi.”
Au “kuhisi mshtuko.”
Au “Nafsi yangu imehuzunika.”
Neno la Kiebrania au Kiaramu linalomaanisha “Ee Baba!”
Au “inapenda.”
Au “akiwa amevaa mavazi machache; akiwa na vazi la ndani tu.”
Au “Mnaonaje?”
Au “sebuleni.”
Au “Auawe kwenye mti!”
Au “Auawe kwenye mti!”
Au “Usifiwe.”
Au “kumwinamia.”
Angalia Kamusi.
Yaani, karibu saa tatu asubuhi.
Angalia Nyongeza A3.
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Yaani, karibu saa 6 mchana.
Yaani, karibu saa 9 alasiri.
Au “akapumua mara ya mwisho.”
Au “kaburi la ukumbusho.”
Au “kwenye kaburi la ukumbusho.”
Kulingana na hati za kale zinazotegemeka, Injili ya Marko inafikia mwisho kwa maneno yaliyo kwenye mstari wa 8. Angalia Nyongeza A3..