Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt 1 Samweli 1:1-31:13
  • 1 Samweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • 1 Samweli
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
1 Samweli

KITABU CHA KWANZA CHA SAMWELI

1 Sasa kulikuwa na mwanamume fulani kutoka Ramathaim-sofimu*+ katika eneo lenye milima la Efraimu+ aliyeitwa Elkana,+ mwana wa Yerohamu, mwana wa Elihu, mwana wa Tohu, mwana wa Sufu, Mwefraimu. 2 Alikuwa na wake wawili, mmoja aliitwa Hana na mwingine aliitwa Penina. Penina alikuwa na watoto, lakini Hana hakuwa na watoto. 3 Mwaka baada ya mwaka mwanamume huyo alitoka katika jiji lake na kupanda kwenda Shilo kumwabudu* na kumtolea dhabihu Yehova wa majeshi.+ Wana wawili wa Eli, Hofni na Finehasi,+ walitumikia huko wakiwa makuhani wa Yehova.+

4 Siku moja Elkana alipotoa dhabihu, alimpa Penina mke wake na wanawe na mabinti zake wote sehemu za dhabihu hiyo,+ 5 lakini akampa Hana sehemu ya pekee, kwa sababu alimpenda sana Hana; lakini Yehova hakuwa amempa watoto.* 6 Isitoshe, mke mwenzake alimdhihaki daima ili kumkasirisha kwa sababu Yehova hakuwa amempa watoto. 7 Hivyo ndivyo alivyofanya mwaka baada ya mwaka; kila mara Hana alipopanda kwenda katika nyumba ya Yehova,+ mke mwenzake alimdhihaki sana hivi kwamba alilia na kushindwa kula. 8 Lakini Elkana mume wake alimuuliza: “Hana, kwa nini unalia, na kwa nini huli chakula, na kwa nini umehuzunika sana?* Je, mimi si bora kwako kuliko wana kumi?”

9 Basi siku moja Hana alisimama baada ya wao kumaliza kula na kunywa huko Shilo. Wakati huo, kuhani Eli alikuwa ameketi kwenye kiti karibu na mwimo wa mlango wa hekalu*+ la Yehova. 10 Hana alikuwa na uchungu mwingi sana,* akaanza kusali kwa Yehova+ na kulia sana. 11 Naye akaweka nadhiri hii: “Ee Yehova wa majeshi, ikiwa utayaona mateso yangu mimi mtumishi wako na kunikumbuka na usiponisahau mimi mtumishi wako, nawe unipe mtoto wa kiume,+ nitamtoa awe wa Yehova sikuzote za maisha yake, na hakuna wembe utakaogusa kichwa chake.”+

12 Alipokuwa akisali kwa muda mrefu mbele za Yehova, Eli alikuwa akiangalia kinywa chake. 13 Hana alikuwa akisali moyoni mwake, midomo yake tu ndiyo iliyokuwa ikitetemeka, lakini sauti yake haikusikika. Basi Eli akafikiri kuwa amelewa. 14 Eli akamwambia, “Utaendelea kuwa mlevi mpaka lini? Acha kunywa divai.” 15 Ndipo Hana akamwambia, “Sivyo, bwana wangu! Mimi ni mwanamke mwenye mkazo mkubwa sana;* sijanywa divai wala kinywaji chochote chenye kileo, bali ninaimwaga nafsi* yangu mbele za Yehova.+ 16 Usidhani mtumishi wako ni mwanamke asiyefaa kitu, kwa maana muda huo wote nimekuwa nikiongea katika uchungu mwingi na mateso yangu.” 17 Ndipo Eli akamwambia, “Nenda kwa amani, na Mungu wa Israeli akupe ulichoomba.”+ 18 Basi Hana akamwambia, “Mtumishi wako na apate kibali machoni pako.” Ndipo mwanamke huyo akaenda zake, akala chakula, na uso wake haukuwa na huzuni tena.

19 Wakaamka asubuhi na mapema na kuinama mbele za Yehova, kisha wakarudi nyumbani kwao kule Rama.+ Elkana akafanya ngono na Hana mke wake, na Yehova akamkumbuka.*+ 20 Katika muda wa mwaka mmoja* Hana alipata mimba, akazaa mwana na kumwita+ mwana huyo Samweli,* kwa maana alisema, “nilimwomba kutoka kwa Yehova.”

21 Baada ya muda Elkana akaenda pamoja na familia yake yote kumtolea Yehova dhabihu+ ya kila mwaka na pia dhabihu yake ya nadhiri. 22 Lakini Hana hakwenda+ kwa sababu alimwambia hivi mume wake: “Mara tu nitakapomwachisha mvulana huyu kunyonya, nitampeleka mbele za Yehova, naye atabaki huko kuanzia wakati huo na kuendelea.”+ 23 Ndipo Elkana mume wake akamwambia, “Fanya unaloona linafaa.* Kaa nyumbani mpaka utakapomwachisha kunyonya. Yehova na atimize jambo ulilosema.” Basi mwanamke huyo akakaa nyumbani, akaendelea kumnyonyesha mwana wake mpaka alipomwachisha kunyonya.

24 Mara tu alipomwachisha kunyonya, alimpeleka Shilo pamoja na ng’ombe dume wa miaka mitatu, efa* moja ya unga, na mtungi mkubwa wa divai,+ naye pamoja na mvulana huyo wakafika katika nyumba ya Yehova huko Shilo.+ 25 Kisha wakamchinja huyo ng’ombe dume na kumpeleka mvulana huyo kwa Eli. 26 Ndipo Hana akasema, “Niwie radhi, bwana wangu! Kwa hakika kama unavyoishi,* bwana wangu, mimi ndiye yule mwanamke aliyekuwa amesimama pamoja nawe mahali hapa ili kusali kwa Yehova.+ 27 Nilisali nipate mvulana huyu, naye Yehova akanipa nilichoomba.+ 28 Sasa nami pia, ninamkabidhi Yehova mvulana huyu. Siku zake zote, amekabidhiwa kwa Yehova.”

Naye* akainama chini mbele za Yehova.

2 Kisha Hana akasema hivi katika sala:

“Moyo wangu unashangilia katika Yehova;+

Pembe yangu imekwezwa* na Yehova.

Kinywa changu kimefunguliwa wazi dhidi ya maadui wangu,

Kwa maana ninashangilia kwa sababu ya matendo yako ya wokovu.

 2 Hakuna aliye mtakatifu kama Yehova,

Hakuna mwingine isipokuwa wewe,+

Na hakuna mwamba kama Mungu wetu.+

 3 Msiendelee kuzungumza kwa kiburi;

Neno lolote la majivuno lisitoke vinywani mwenu,

Kwa maana Yehova ni Mungu wa ujuzi,+

Naye hupima matendo kwa njia ya haki.

 4 Pinde za mashujaa huvunjwavunjwa,

Lakini wale wanaojikwaa hutiwa nguvu.+

 5 Walioshiba lazima waajiriwe ili wapate mkate,

Lakini wenye njaa hawana njaa tena.+

Aliye tasa amezaa watoto saba,+

Lakini mwanamke aliyekuwa na wana wengi ameachwa mpweke.*

 6 Yehova huua, naye huhifadhi uhai;*

Hushusha Kaburini,* naye hufufua.+

 7 Yehova humfanya mtu awe maskini, naye hutajirisha;+

Hushusha, naye hukweza.+

 8 Humwinua mtu wa hali ya chini kutoka mavumbini;

Humwinua maskini kutoka katika rundo la majivu,*+

Ili awafanye wakae pamoja na wakuu,

Na kuwapa kiti cha heshima.

Nguzo za dunia ni za Yehova,+

Naye huweka nchi inayozaa juu yake.

 9 Hulinda hatua za washikamanifu wake;+

Lakini waovu watanyamazishwa gizani,+

Kwa maana mwanadamu hashindi kwa nguvu.+

10 Yehova atawavunjavunja wale wanaopigana naye;*+

Atanguruma dhidi yao kutoka mbinguni.+

Yehova atahukumu mpaka miisho ya dunia,+

Atampa nguvu mfalme wake,+

Na kuikweza pembe ya* mtiwa-mafuta wake.”+

11 Basi Elkana akaenda nyumbani kwake Rama, lakini yule mvulana akawa mhudumu wa* Yehova+ chini ya uangalizi wa kuhani Eli.

12 Sasa wana wa Eli walikuwa watu waovu;+ hawakumheshimu Yehova. 13 Hivi ndivyo walivyofanya kuhusu vitu vilivyoletwa na watu ambavyo vilikuwa haki ya makuhani:+ Kila mara mtu yeyote alipokuwa akitoa dhabihu, mtumishi wa kuhani alikuja na uma wenye meno matatu mkononi mwake nyama ilipokuwa ikichemka, 14 naye aliutia kwa nguvu ndani ya beseni, chungu cha kupikia chenye mikono miwili, sufuria kubwa, au chungu cha kupikia chenye mkono mmoja. Nyama yoyote iliyoinuliwa na uma huo, ilichukuliwa na kuhani. Hivyo ndivyo walivyokuwa wakiwatendea Waisraeli wote waliokuja Shilo. 15 Pia, hata kabla ya mtu anayetoa dhabihu kuyafanya mafuta yafuke moshi,+ mtumishi wa kuhani alikuwa akija na kumwambia, “Mpe kuhani nyama akachome. Hatachukua nyama iliyochemshwa kutoka kwako, atachukua nyama mbichi tu.” 16 Mtu huyo alipomwambia, “Acha kwanza wahakikishe kwamba mafuta yamefuka moshi,+ kisha ujichukulie chochote upendacho,”* alisema: “Hapana, nipe sasa hivi; la sivyo, nitaichukua kwa nguvu!” 17 Kwa hiyo dhambi ya watumishi hao ikawa kubwa sana mbele za Yehova,+ kwa maana watu hao hawakuheshimu dhabihu ya Yehova.

18 Basi Samweli alikuwa akihudumu+ mbele za Yehova, akiwa amevaa* efodi ya kitani,+ ingawa alikuwa mvulana tu. 19 Pia, mama yake alikuwa akimshonea joho dogo lisilo na mikono na kumletea mwaka baada ya mwaka alipokuja na mume wake kutoa dhabihu ya kila mwaka.+ 20 Eli akambariki Elkana na mke wake akisema, “Yehova na akupe mtoto kutoka kwa mke huyu ili achukue nafasi ya yule aliyekabidhiwa kwa Yehova.”+ Kisha wakarudi nyumbani. 21 Yehova akamkazia uangalifu Hana, ili aweze kupata mimba;+ basi akazaa wana watatu zaidi na mabinti wawili. Naye mvulana Samweli akaendelea kukua mbele za Yehova.+

22 Sasa Eli alikuwa amezeeka sana, lakini alikuwa amesikia mambo yote ambayo wanawe walikuwa wakiwatendea+ Waisraeli wote na jinsi walivyokuwa wakilala na wanawake waliotumikia kwenye mlango wa hema la mkutano.+ 23 Alikuwa akiwaambia hivi: “Kwa nini mnaendelea kufanya mambo ya aina hii? Kwa maana mambo ninayosikia kuwahusu kutoka kwa watu wote ni mabaya. 24 Msifanye hivyo wanangu, kwa sababu habari ninazosikia zikienea miongoni mwa watu wa Yehova si nzuri. 25 Mwanadamu akimtendea dhambi mwanadamu mwenzake, mtu fulani anaweza kumsihi Yehova kwa niaba yake;* lakini mwanadamu akimtendea dhambi Yehova,+ ni nani anayeweza kusali kwa ajili yake?” Lakini walikataa kumsikiliza baba yao, kwa sababu Yehova alikuwa ameazimia kuwaua.+ 26 Lakini mvulana Samweli aliendelea kukua na kupendwa na Yehova na pia wanadamu.+

27 Mtu wa Mungu alimjia Eli na kumwambia, “Yehova anasema hivi: ‘Je, sikujitambulisha waziwazi kwa watu wa nyumba ya baba yako walipokuwa Misri wakiwa watumwa wa nyumba ya Farao?+ 28 Naye alichaguliwa kutoka katika makabila yote ya Israeli+ ili anitumikie akiwa kuhani wangu na kupanda juu ya madhabahu yangu+ kutoa dhabihu, kufukiza uvumba,* na kuvaa efodi mbele zangu; nami niliwapa watu wa nyumba ya babu yako dhabihu zote zinazochomwa kwa moto zilizotolewa na Waisraeli.*+ 29 Kwa nini ninyi wanaume mnadharau* dhabihu yangu na toleo langu ambalo nimeamuru katika makao yangu?+ Kwa nini unaendelea kuwaheshimu wana wako kuliko mimi kwa kujinenepesha kwa sehemu bora za kila dhabihu inayotolewa na watu wangu Waisraeli?+

30 “‘Ndiyo sababu Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: “Hakika nilisema kwamba nyumba yako na nyumba ya babu yako itatembea mbele zangu daima.”+ Lakini sasa Yehova anatangaza hivi: “Ni jambo nisiloweza kamwe kuwazia, kwa sababu wale wanaoniheshimu nitawaheshimu,+ lakini wale wanaonidharau watadharauliwa.” 31 Tazama! Siku zinakuja nitakapokata nguvu zako na za* nyumba ya baba yako, hivi kwamba hakuna mwanamume yeyote wa nyumba yako atakayeishi na kuzeeka.+ 32 Nawe utamwona adui katika makao yangu miongoni mwa mambo yote mema wanayofanyiwa Waisraeli,+ na kamwe hakutakuwa tena na mzee katika nyumba yako. 33 Mwanamume wako ambaye nitamwacha aendelee kutumikia kwenye madhabahu yangu atayadhoofisha macho yako na kukuletea huzuni, lakini idadi kubwa ya watu wa nyumba yako itauawa kwa upanga.+ 34 Na mambo yatakayowapata wana wako wawili, Hofni na Finehasi, yatakuwa ishara kwako: Wote wawili watakufa siku ileile.+ 35 Kisha nitajiinulia kuhani mwaminifu.+ Atatenda kulingana na mapenzi ya moyo wangu;* nami nitamjengea nyumba ya kudumu, naye atatembea mbele ya mtiwa-mafuta wangu daima. 36 Mtu yeyote atakayebaki katika nyumba yako atakuja na kumwinamia ili alipwe pesa na kupata mkate, naye atasema: “Tafadhali, niweke katika nafasi yoyote ya ukuhani ili nile kipande cha mkate.”’”+

3 Wakati huo, mvulana Samweli alikuwa akimhudumia+ Yehova chini ya uangalizi wa Eli, lakini neno la Yehova lilikuwa haba siku hizo; maono+ hayakuwa mengi.

2 Siku moja Eli alikuwa amelala mahali alipozoea kulala, na macho yake yalikuwa yamedhoofika; hangeweza kuona.+ 3 Taa ya Mungu+ haikuwa imezimwa, na Samweli alikuwa amelala katika hekalu*+ la Yehova, mahali ambapo Sanduku la Mungu lilikuwa. 4 Kisha Yehova akamwita Samweli. Samweli akajibu: “Mimi hapa.” 5 Akakimbia kwa Eli na kusema, “Nimekuja, kwa kuwa umeniita.” Lakini Eli akasema: “Sikukuita. Rudi ukalale.” Basi akaenda kulala. 6 Yehova akaita tena: “Samweli!” Basi Samweli akaamka na kwenda kwa Eli, akamwambia: “Nimekuja, kwa kuwa umeniita.” Lakini Eli akamwambia: “Sikukuita, mwanangu. Rudi ukalale.” 7 (Wakati huo Samweli alikuwa bado hajamjua Yehova, na neno la Yehova lilikuwa bado halijafunuliwa kwake.)+ 8 Yehova akaita tena mara ya tatu: “Samweli!” Basi akaamka, akaenda kwa Eli na kumwambia: “Nimekuja, kwa kuwa umeniita.”

Ndipo Eli akatambua kwamba ni Yehova aliyekuwa akimwita mvulana huyo. 9 Kwa hiyo Eli akamwambia Samweli: “Rudi ukalale, na akikuita, mwambie, ‘Sema, Yehova, kwa maana mtumishi wako anasikiliza.’” Basi Samweli akaenda na kulala mahali alipokuwa akilala.

10 Yehova akaja na kusimama mahali hapo, akaita kama alivyofanya awali: “Samweli, Samweli!” Ndipo Samweli akajibu: “Sema, kwa maana mtumishi wako anasikiliza.” 11 Yehova akamwambia Samweli: “Tazama! Ninafanya jambo fulani katika Israeli ambalo litawasha masikio yote mawili ya mtu yeyote atakayelisikia.+ 12 Siku hiyo nitamtendea Eli mambo yote niliyosema kuhusu nyumba yake, kuanzia mwanzo mpaka mwisho.+ 13 Ni lazima umwambie kwamba ninailetea nyumba yake hukumu ya kudumu kwa sababu ya dhambi ambayo anaijua,+ kwa maana wanawe wanamtukana Mungu,+ lakini hajawakemea.+ 14 Ndiyo sababu nimeiapia nyumba ya Eli kwamba dhambi ya nyumba ya Eli haitafunikwa kamwe kwa dhabihu au kwa matoleo.”+

15 Samweli akaendelea kulala mpaka asubuhi; kisha akafungua milango ya nyumba ya Yehova. Samweli akaogopa kumwambia Eli maono hayo. 16 Lakini Eli akaagiza Samweli aitwe, akamwambia: “Samweli, mwanangu!” Naye akasema: “Naam.”⁠ 17 Eli akamuuliza, “Alikupa ujumbe gani? Tafadhali, usinifiche. Mungu na akuadhibu, tena vikali, ukinificha neno hata moja kati ya maneno yote ambayo alikwambia.” 18 Basi Samweli akamwambia kila jambo, wala hakumficha lolote. Eli akasema: “Ni Yehova. Na afanye yaliyo mema machoni pake.”

19 Samweli akaendelea kukua, na Yehova mwenyewe alikuwa pamoja naye+ na hakuruhusu neno lolote kati ya maneno yake yote likose kutimia.* 20 Waisraeli wote kuanzia Dani mpaka Beer-sheba wakapata habari kwamba Samweli alikuwa amewekwa rasmi kuwa nabii wa Yehova. 21 Na Yehova akaendelea kutokea huko Shilo, kwa kuwa Yehova alijidhihirisha kwa Samweli huko Shilo kwa neno lake Yehova.+

4 Na neno la Samweli likawafikia Waisraeli wote.

Kisha Waisraeli wakaenda kupigana na Wafilisti; wakapiga kambi kando ya Ebenezeri, na Wafilisti walikuwa wamepiga kambi Afeki. 2 Wafilisti wakajipanga kivita ili kupigana na Waisraeli, lakini mambo yakawaendea vibaya Waisraeli vitani, nao wakashindwa na Wafilisti, ambao waliwaua wanaume wapatao 4,000 kwenye uwanja wa vita. 3 Watu waliporudi kambini, wazee wa Israeli wakasema hivi: “Kwa nini Yehova ameruhusu tushindwe leo na Wafilisti?*+ Na tujichukulie sanduku la agano la Yehova kutoka Shilo,+ twende nalo ili lituokoe kutoka mikononi mwa maadui wetu.” 4 Basi watu wakawatuma wanaume kwenda Shilo, nao wakachukua kutoka huko sanduku la agano la Yehova wa majeshi, anayeketi akiwa mfalme juu ya* makerubi.+ Na wana wawili wa Eli, yaani, Hofni na Finehasi,+ walikuwa huko pia pamoja na sanduku la agano la Mungu wa kweli.

5 Mara tu sanduku la agano la Yehova lilipofika kambini, Waisraeli wote wakaanza kupiga kelele kwa sauti kubwa, hivi kwamba dunia ikatikisika. 6 Wafilisti waliposikia kelele hizo, wakasema: “Kwa nini kuna kelele nyingi sana katika kambi ya Waebrania?” Hatimaye wakapata habari kwamba Sanduku la Yehova lilikuwa limeletwa kambini. 7 Wafilisti wakaogopa, kwa sababu walisema: “Mungu amekuja kambini!”+ Basi wakasema: “Ole wetu, kwa maana jambo kama hili halijawahi kamwe kutokea! 8 Ole wetu! Ni nani atakayetuokoa kutoka katika mkono wa Mungu huyu mkuu? Huyu ndiye Mungu aliyewachinja Wamisri kwa kila aina ya mapigo nyikani.+ 9 Iweni jasiri na kutenda kama wanaume, enyi Wafilisti, ili msiwatumikie Waebrania kama walivyowatumikia ninyi.+ Tendeni kama wanaume, mkapigane!” 10 Basi Wafilisti wakapigana nao, na Waisraeli wakashindwa,+ na kila mmoja wao akakimbilia katika hema lake. Yalikuwa mauaji makubwa sana; wanajeshi 30,000 wa Israeli wanaotembea kwa miguu waliuawa. 11 Isitoshe, Sanduku la Mungu lilitekwa, na wana wawili wa Eli, Hofni na Finehasi, wakafa.+

12 Mtu fulani Mbenjamini akakimbia kutoka katika uwanja wa vita, akafika Shilo siku hiyo akiwa amevaa nguo zilizoraruka na akiwa na mavumbi kichwani.+ 13 Mtu huyo alipofika, Eli alikuwa ameketi kwenye kiti kando ya barabara akitazama barabarani, kwa kuwa moyo wake ulikuwa ukitetemeka kwa sababu ya Sanduku la Mungu wa kweli.+ Mtu huyo akaingia jijini kutangaza habari hizo, na jiji lote likaanza kulia kwa sauti kubwa. 14 Eli aliposikia vilio hivyo, akauliza: “Kelele hizo za machafuko ni za nini?” Mtu huyohuyo akafika haraka na kumwambia Eli habari hizo. 15 (Wakati huo Eli alikuwa na umri wa miaka 98, naye alikodoa macho yake mbele, lakini hakuweza kuona.)+ 16 Kisha mtu huyo akamwambia Eli: “Ni mimi niliyetoka katika uwanja wa vita! Nimekimbia kutoka katika uwanja wa vita leo hii.” Basi akamuuliza: “Mwanangu, ilikuwaje?” 17 Basi mtu huyo aliyeleta habari akasimulia hivi: “Waisraeli wamewakimbia Wafilisti, na watu wameshindwa vibaya sana;+ pia, wana wako wawili, Hofni na Finehasi, wamekufa,+ na Sanduku la Mungu wa kweli limetekwa.”+

18 Mara tu alipotaja Sanduku la Mungu wa kweli, Eli akaanguka nyuma kutoka kwenye kiti chake kando ya lango, na shingo yake ikavunjika naye akafa, kwa sababu alikuwa amezeeka na alikuwa mzito. Alikuwa mwamuzi wa Israeli kwa miaka 40. 19 Binti mkwe wake, yaani, mke wa Finehasi, alikuwa mjamzito naye alikuwa karibu kuzaa. Aliposikia kwamba Sanduku la Mungu wa kweli limetekwa na kwamba baba mkwe wake na mume wake wamekufa, akainama na kwa ghafla akapata uchungu wa kuzaa, kisha akazaa. 20 Alipokuwa akifa, wanawake waliokuwa wamesimama kando yake wakasema: “Usiogope, kwa maana umezaa mwana.” Hakujibu wala kukazia fikira jambo hilo.* 21 Lakini alimwita mvulana huyo Ikabodi,*+ akisema: “Utukufu umeondoka Israeli na kwenda uhamishoni,”+ alisema hivyo kwa sababu Sanduku la Mungu wa kweli lilitekwa na kwa sababu ya mambo yaliyompata baba mkwe wake na mume wake.+ 22 Basi akasema: “Utukufu umeondoka Israeli na kwenda uhamishoni, kwa sababu Sanduku la Mungu wa kweli limetekwa.”+

5 Wafilisti walipoliteka Sanduku la Mungu+ wa kweli walilibeba kutoka Ebenezeri mpaka Ashdodi. 2 Wafilisti wakalichukua Sanduku la Mungu wa kweli, wakaliingiza ndani ya nyumba ya* Dagoni na kuliweka kando ya Dagoni.+ 3 Siku iliyofuata Waashdodi walipoamka asubuhi na mapema, walimkuta Dagoni ameanguka kifudifudi mbele ya Sanduku la Yehova.+ Basi wakamchukua Dagoni na kumrudisha mahali pake.+ 4 Walipoamka asubuhi na mapema siku iliyofuata, walimkuta Dagoni ameanguka kifudifudi mbele ya Sanduku la Yehova. Kichwa cha Dagoni na vitanga vya mikono yake miwili vilikuwa vimekatwa, navyo vilikuwa chini kwenye kizingiti. Ni sehemu tu yenye umbo la samaki ndiyo iliyobaki.* 5 Ndiyo sababu mpaka leo hii, makuhani wa Dagoni na wote wanaoingia katika nyumba ya Dagoni hawakanyagi kizingiti cha Dagoni kule Ashdodi.

6 Mkono wa Yehova uliwaadhibu vikali* Waashdodi, naye akawaangamiza kwa kuleta bawasiri* huko Ashdodi na katika maeneo yake.+ 7 Watu wa Ashdodi walipoona mambo yaliyokuwa yakitukia wakasema: “Msiruhusu Sanduku la Mungu wa Israeli likae pamoja nasi, kwa sababu mkono wake umetuadhibu vikali sisi pamoja na mungu wetu Dagoni.” 8 Basi wakatuma ujumbe na kuwakusanya watawala wote wa Wafilisti na kuwauliza: “Tulifanyie nini Sanduku la Mungu wa Israeli?” Wakajibu: “Acheni Sanduku la Mungu wa Israeli lihamishiwe kule Gathi.”+ Basi wakalihamishia huko Sanduku la Mungu wa Israeli.

9 Baada ya kulihamishia huko, mkono wa Yehova ukaja dhidi ya jiji hilo, na kusababisha hofu kubwa. Akawapiga wanaume wa jiji hilo, kuanzia mdogo mpaka mkubwa, wakatokwa na majipu ya bawasiri.+ 10 Basi wakalipeleka Sanduku la Mungu wa kweli kule Ekroni,+ lakini mara tu Sanduku la Mungu wa kweli lilipofika Ekroni, Waekroni wakaanza kulia kwa sauti wakisema: “Wametuletea Sanduku la Mungu wa Israeli ili watuue sisi pamoja na watu wetu!”+ 11 Kwa hiyo wakatuma ujumbe na kuwakusanya watawala wote wa Wafilisti na kuwaambia: “Liondoeni hapa Sanduku la Mungu wa Israeli; lirudisheni mahali pake ili sisi pamoja na watu wetu tusiuawe.” Kwa maana hofu ya kifo ilikuwa imeenea katika jiji lote; mkono wa Mungu wa kweli ulikuwa umewaadhibu vikali sana watu wa jiji hilo,+ 12 na watu ambao hawakufa walikuwa wamepigwa na bawasiri. Na kilio cha jiji hilo cha kuomba msaada kikapanda mpaka mbinguni.

6 Sanduku+ la Yehova lilikaa katika eneo la Wafilisti kwa miezi saba. 2 Wafilisti wakawaita makuhani na wabashiri,+ wakawauliza: “Tulifanyie nini Sanduku la Yehova? Tuambieni jinsi tunavyopaswa kulirudisha mahali pake.” 3 Wakajibu: “Mkilirudisha sanduku la agano la Yehova, Mungu wa Israeli, msilirudishe bila dhabihu. Kwa vyovyote vile mnapaswa kumrudishia pamoja na dhabihu ya hatia.+ Ndipo tu mtakapoponywa, nanyi mtajulishwa kwa nini mkono wake unaendelea kuwaadhibu.” 4 Basi wakauliza: “Tunapaswa kumpelekea dhabihu gani ya hatia?” Wakasema: “Kulingana na idadi ya watawala wa Wafilisti,+ pelekeni bawasiri tano za dhahabu na panya watano wa dhahabu, kwa maana kila mmoja wenu pamoja na watawala wenu wamepatwa na pigo lilelile. 5 Mnapaswa kutengeneza sanamu za bawasiri zenu na sanamu za panya+ wenu wanaoiharibu nchi, nanyi mnapaswa kumheshimu Mungu wa Israeli. Labda atapunguza adhabu ya mkono wake dhidi yenu na dhidi ya mungu wenu na nchi yenu.+ 6 Kwa nini mfanye mioyo yenu iwe migumu kama Wamisri na Farao walivyofanya mioyo yao kuwa migumu?+ Alipowaadhibu vikali,+ walilazimika kuwaruhusu Waisraeli waende zao, nao wakaondoka.+ 7 Sasa tayarisheni gari jipya la kukokotwa na ng’ombe wawili wanaonyonyesha ambao hawajawahi kamwe kufungwa nira. Kisha muwafunge ng’ombe hao kwenye gari hilo, lakini muwarudishe ndama wao nyumbani ili wasiwafuate. 8 Chukueni Sanduku la Yehova na kuliweka juu ya gari hilo, nanyi wekeni ndani ya sanduku lingine kando yake vitu vya dhahabu mnavyompelekea kuwa dhabihu ya hatia.+ Kisha mliache gari liende 9 huku mkilitazama: Ikiwa litapanda kwenye barabara inayoelekea Beth-shemeshi,+ kwenye eneo lake, basi yeye ndiye ametutendea uovu huu mkubwa. Lakini lisipopanda huko, tutajua kwamba si mkono wake uliotuadhibu; ni msiba wa kawaida tu uliotupata.”

10 Watu hao wakafanya hivyo. Wakachukua ng’ombe wawili wanaonyonyesha, wakawafunga kwenye gari hilo, na kuwafungia ndama wao nyumbani ndani ya zizi. 11 Kisha wakaliweka Sanduku la Yehova juu ya gari hilo, pamoja na sanduku lenye panya wa dhahabu na sanamu za bawasiri zao. 12 Ng’ombe hao wakaenda moja kwa moja kwenye barabara inayoelekea Beth-shemeshi.+ Walibaki kwenye barabara hiyo kuu, nao walikuwa wakilia walipokuwa wakienda; hawakugeuka kulia wala kushoto. Wakati huo wote, watawala wa Wafilisti walikuwa wakitembea nyuma yao hadi kwenye mpaka wa Beth-shemeshi. 13 Watu wa Beth-shemeshi walikuwa wakivuna ngano katika bonde tambarare. Walipoinua macho yao na kuona lile Sanduku, wakashangilia sana kuliona. 14 Gari hilo likafika kwenye shamba la Yoshua Mbeth-shemeshi, likasimama karibu na jiwe kubwa. Basi wakapasua mbao za gari hilo, na kuwatoa ng’ombe+ hao kuwa dhabihu ya kuteketezwa kwa Yehova.

15 Walawi+ wakalishusha Sanduku la Yehova na sanduku lililokuwa kando yake ambalo lilikuwa na vile vitu vya dhahabu, wakaviweka juu ya lile jiwe kubwa. Watu wa Beth-shemeshi+ wakamtolea Yehova dhabihu za kuteketezwa na dhabihu nyingine siku hiyo.

16 Watawala watano wa Wafilisti walipoona hayo, wakarudi Ekroni siku hiyo. 17 Basi hizi ndizo bawasiri za dhahabu ambazo Wafilisti walimletea Yehova kuwa dhabihu ya hatia:+ moja kwa ajili ya Ashdodi,+ moja kwa ajili ya Gaza, moja kwa ajili ya Ashkeloni, moja kwa ajili ya Gathi,+ moja kwa ajili ya Ekroni.+ 18 Na idadi ya panya wa dhahabu ililingana na idadi ya majiji yote ya Wafilisti ya wale watawala watano, majiji yenye ngome na vijiji vya mashambani visivyo na kuta.

Na jiwe kubwa ambalo waliweka Sanduku la Yehova juu yake ni ushahidi mpaka leo katika shamba la Yoshua Mbeth-shemeshi. 19 Lakini Mungu akawaua watu wa Beth-shemeshi, kwa sababu walilitazama Sanduku la Yehova. Aliwaua watu 50,070* miongoni mwao, basi watu wakaanza kuomboleza kwa sababu Yehova alikuwa amewaua kwa mauaji makubwa.+ 20 Kwa hiyo watu wa Beth-shemeshi wakauliza: “Ni nani atakayeweza kusimama mbele za Yehova, huyu Mungu mtakatifu,+ naye ataenda kwa nani akitoka kwetu?”+ 21 Basi wakawatuma wajumbe kwa wakaaji wa Kiriath-yearimu,+ wakisema: “Wafilisti wamelirudisha Sanduku la Yehova. Shukeni mlichukue na kupanda nalo.”+

7 Basi watu wa Kiriath-yearimu wakaja na kulichukua Sanduku la Yehova na kulipandisha katika nyumba ya Abinadabu+ juu ya kilima, nao wakamtakasa Eleazari mwanawe ili alilinde Sanduku la Yehova.

2 Muda mrefu ulipita, jumla ya miaka 20, tangu Sanduku hilo lilipoletwa Kiriath-yearimu, na nyumba yote ya Israeli kuanza kumtafuta* Yehova.+ 3 Kisha Samweli akaiambia nyumba yote ya Israeli: “Ikiwa mnamrudia Yehova kwa moyo wenu wote,+ ondoeni miungu ya kigeni+ na sanamu za Ashtorethi+ kutoka kati yenu, nanyi elekezeni moyo wenu kwa Yehova bila kuyumbayumba na kumtumikia yeye peke yake,+ naye atawaokoa kutoka mikononi mwa Wafilisti.”+ 4 Kwa hiyo Waisraeli wakaondoa Mabaali na sanamu za Ashtorethi na kumtumikia Yehova peke yake.+

5 Kisha Samweli akasema: “Wakusanyeni Waisraeli wote Mispa,+ nami nitasali kwa Yehova kwa ajili yenu.”+ 6 Basi wakakusanyika pamoja huko Mispa, nao wakachota maji na kuyamwaga mbele za Yehova na kufunga siku hiyo.+ Wakiwa huko wakasema: “Tumemtendea dhambi Yehova.”+ Naye Samweli akaanza kutumikia akiwa mwamuzi+ wa Waisraeli huko Mispa.

7 Wafilisti waliposikia kwamba Waisraeli wamekusanyika pamoja Mispa, watawala wa Wafilisti+ wakapanda kwenda kuwashambulia Waisraeli. Waisraeli waliposikia habari hizo, waliogopa kwa sababu ya Wafilisti. 8 Kwa hiyo Waisraeli wakamwambia Samweli: “Usiache kumwomba Yehova Mungu wetu atusaidie+ na kutuokoa kutoka mikononi mwa Wafilisti.” 9 Ndipo Samweli akachukua mwanakondoo anayenyonya, akamtoa kwa Yehova kuwa dhabihu nzima ya kuteketezwa;+ na Samweli akamwomba Yehova awasaidie Waisraeli, naye Yehova akamjibu.+ 10 Samweli alipokuwa akitoa dhabihu hiyo ya kuteketezwa, Wafilisti wakakaribia ili kupigana na Waisraeli. Basi siku hiyo Yehova akawaletea Wafilisti mngurumo mkubwa sana,+ Naye akawavuruga,+ wakashindwa mbele ya Waisraeli.+ 11 Ndipo wanaume wa Israeli wakatoka Mispa na kuwafuatia Wafilisti, wakawaua mpaka upande wa kusini wa Beth-kari. 12 Kisha Samweli akachukua jiwe+ na kuliweka kati ya Mispa na Yeshana, akaliita Ebenezeri,* kwa kuwa alisema: “Yehova ametusaidia mpaka sasa.”+ 13 Kwa hiyo Wafilisti wakashindwa, nao hawakuja tena katika eneo la Waisraeli;+ na mkono wa Yehova ukaendelea kuwashinda Wafilisti siku zote za Samweli.+ 14 Pia, majiji ambayo Wafilisti walikuwa wamechukua kutoka kwa Waisraeli yalirudishwa kwa Waisraeli, kuanzia Ekroni mpaka Gathi, na Waisraeli wakayakomboa maeneo yao kutoka mikononi mwa Wafilisti.

Pia kukawa na amani kati ya Waisraeli na Waamori.+

15 Samweli akaendelea kuwa mwamuzi wa Israeli maisha yake yote.+ 16 Kila mwaka alisafiri na kuzunguka Betheli,+ Gilgali,+ na Mispa,+ naye alikuwa mwamuzi wa Israeli katika maeneo hayo yote. 17 Lakini alikuwa akirudi Rama,+ kwa sababu nyumba yake ilikuwa huko, na huko pia alitumikia akiwa mwamuzi wa Israeli. Alimjengea Yehova madhabahu huko.+

8 Samweli alipokuwa amezeeka, aliwaweka wanawe kuwa waamuzi wa Israeli. 2 Mwana wake wa kwanza aliitwa Yoeli, na wa pili aliitwa Abiya;+ walikuwa waamuzi huko Beer-sheba. 3 Lakini wanawe hawakufuata njia zake; walikuwa na mwelekeo wa kujitafutia faida isiyo ya haki,+ walipokea rushwa,+ na kupotosha haki.+

4 Baada ya muda wazee wote wa Waisraeli walikusanyika pamoja na kuja kumwona Samweli huko Rama. 5 Wakamwambia: “Tazama! Umezeeka, lakini wana wako hawatembei katika njia zako. Basi tuchagulie mfalme awe mwamuzi wetu kama mataifa mengine yote.”+ 6 Lakini Samweli hakufurahi waliposema: “Tupe mfalme awe mwamuzi wetu.” Kwa hiyo Samweli akasali kwa Yehova, 7 Yehova akamwambia Samweli: “Sikiliza mambo yote ambayo watu wanakuambia; kwa maana hawajakukataa wewe, bali wamenikataa mimi nisiwe mfalme wao.+ 8 Wanatenda kama walivyozoea kutenda tangu nilipowatoa Misri mpaka leo hii; wamekuwa wakiniacha+ na kuabudu miungu mingine,+ na hivyo ndivyo wanavyokutendea wewe pia. 9 Sasa wasikilize. Hata hivyo, unapaswa kuwaonya vikali; waambie mambo ambayo mfalme atakayewatawala atakuwa na haki ya kudai.”

10 Basi Samweli akawaambia maneno yote ya Yehova watu waliokuwa wakimwomba awape mfalme. 11 Akasema: “Mfalme atakayewatawala atakuwa na haki ya kudai mambo haya:+ Atawachukua wana wenu+ na kuwafanya wawe waendeshaji wa magari yake ya farasi+ na wapanda farasi wake,+ na baadhi yao watalazimika kukimbia mbele ya magari yake. 12 Naye atajichagulia wakuu wa maelfu+ na wakuu wa hamsini,+ na baadhi yao watamlimia mashamba yake,+ watavuna mazao yake,+ na kutengeneza silaha zake za vita na vifaa vya magari yake.+ 13 Atachukua mabinti wenu na kuwafanya kuwa watengenezaji wa marashi,* wapishi, na waokaji.+ 14 Atachukua mashamba yenu bora, mashamba yenu bora ya mizabibu, na mashamba yenu bora ya mizeituni+ na kuwapa watumishi wake. 15 Atachukua sehemu ya kumi ya mashamba yenu ya nafaka na mashamba yenu ya mizabibu na kuwapa maofisa wa makao yake na watumishi wake. 16 Naye atachukua watumishi wenu wa kiume na wa kike, ng’ombe wenu walio bora, na punda wenu na kuwatumia kufanya kazi zake.+ 17 Atachukua sehemu ya kumi ya kondoo wenu na mbuzi wenu,+ nanyi mtakuwa watumishi wake. 18 Siku itafika mtakapolia kwa sababu ya mfalme ambaye mlijichagulia wenyewe,+ lakini Yehova hatawajibu siku hiyo.”

19 Hata hivyo, watu wakakataa kusikiliza mambo ambayo Samweli aliwaambia, wakasema: “Hatutaki, tumeazimia kuwa na mfalme wa kututawala. 20 Kisha tutakuwa kama mataifa mengine yote, na mfalme wetu atakuwa mwamuzi wetu, atatuongoza, na kupigana vita vyetu.” 21 Baada ya Samweli kusikia maneno yote ya watu, akayarudia masikioni mwa Yehova. 22 Yehova akamwambia Samweli: “Wasikilize, na uweke mfalme wa kuwatawala.”+ Basi Samweli akawaambia Waisraeli: “Kila mmoja wenu arudi katika jiji lake.”

9 Kulikuwa na mtu wa Benjamini aliyeitwa Kishi,+ mwana wa Abieli, mwana wa Zerori mwana wa Bekorathi mwana wa Afia, Mbenjamini+ aliyekuwa tajiri sana. 2 Alikuwa na mwana aliyeitwa Sauli,+ kijana mwenye sura nzuri, hakuna mwanamume yeyote kati ya Waisraeli aliyekuwa na sura nzuri kuliko yeye, na aliposimama watu wote walimfikia mabegani.

3 Punda wa Kishi baba ya Sauli walipopotea, Kishi alimwambia hivi Sauli mwanawe: “Tafadhali mchukue mtumishi mmoja mwende mkawatafute punda.” 4 Wakapita katika eneo lenye milima la Efraimu na katika nchi ya Shalisha, lakini hawakuwapata. Wakasafiri kupitia nchi ya Shaalimu, lakini hawakuwapata punda huko. Wakapita katika nchi yote ya Wabenjamini, lakini hawakuwapata.

5 Wakafika katika nchi ya Sufu, Sauli akamwambia mtumishi wake aliyekuwa pamoja naye: “Njoo, acha turudi, ili baba yangu asianze kutuhangaikia badala ya kuhangaikia punda.”+ 6 Lakini mtumishi huyo akamwambia: “Tazama! Kuna mtu wa Mungu katika jiji hili, mtu anayeheshimiwa. Kila jambo analosema lazima litimie.+ Twende huko sasa. Labda anaweza kutuambia njia ya kufuata.” 7 Basi Sauli akamwambia hivi mtumishi wake: “Tukienda, tutampelekea nini mtu huyo? Mifuko yetu haina mikate; hatuna zawadi yoyote ya kumpelekea huyo mtu wa Mungu wa kweli. Tuna nini?” 8 Basi mtumishi huyo akamjibu hivi Sauli: “Tazama! Nimebeba mikononi mwangu robo ya shekeli* ya fedha. Nitampa huyo mtu wa Mungu wa kweli, naye atatuambia njia ya kufuata.” 9 (Zamani katika Israeli, mtu alikuwa akisema hivi alipoenda kutafuta mwongozo wa Mungu: “Njoo, twende kwa mwonaji.”+ Kwa maana mtu ambaye leo anaitwa nabii, zamani aliitwa mwonaji.) 10 Ndipo Sauli akamwambia hivi mtumishi wake: “Ulilosema ni jema. Haya twende.” Basi wakaenda katika jiji alimokuwa yule mtu wa Mungu wa kweli.

11 Walipokuwa wakipanda kwenda jijini, walikutana na wasichana waliokuwa wakienda kuteka maji. Basi wakawauliza: “Je, mwonaji+ yuko katika jiji hili?” 12 Wakajibu: “Ndiyo. Hajafika mbali sana. Fanyeni haraka, kwa sababu amekuja jijini leo, kwa maana leo watu wanatoa dhabihu+ mahali pa juu.+ 13 Mara tu mtakapoingia jijini, mtamkuta kabla hajapanda kwenda mahali pa juu kula chakula. Watu hawatakula mpaka atakapofika, kwa maana yeye ndiye anayebariki dhabihu. Baada ya kufanya hivyo, wale walioalikwa wanaweza kula. Basi pandeni sasa moja kwa moja, mtamkuta.” 14 Basi wakapanda kwenda jijini. Walipokuwa wakiingia katikati ya jiji, Samweli alikuwa akija kukutana nao akielekea mahali pa juu.

15 Siku iliyotangulia kabla ya Sauli kufika, Yehova alikuwa amemwambia* Samweli: 16 “Kesho wakati kama huu, nitatuma mtu kwako kutoka katika nchi ya Benjamini.+ Utamtia mafuta awe kiongozi juu ya watu wangu Waisraeli,+ naye atawaokoa watu wangu kutoka mikononi mwa Wafilisti. Kwa sababu nimeyaona mateso ya watu wangu, na kilio chao kimenifikia.”+ 17 Samweli alipomwona Sauli, Yehova akamwambia: “Huyu ndiye mtu niliyekwambia, ‘Yeye ndiye atakayewaongoza watu wangu.’”*+

18 Kisha Sauli akamkaribia Samweli katikati ya lango na kumuuliza: “Tafadhali niambie, nyumba ya mwonaji iko wapi?” 19 Samweli akamjibu Sauli: “Mimi ndiye mwonaji. Panda utangulie mbele yangu mahali pa juu, nawe utakula pamoja nami leo.+ Asubuhi nitakuruhusu uende, nami nitakueleza mambo yote unayotaka kujua.* 20 Kuhusu wale punda waliopotea siku tatu zilizopita,+ usiwe na wasiwasi juu yao, kwa maana wamepatikana. Vitu vyote vyenye kutamanika vya Israeli ni vya nani? Je, si vyako na vya nyumba yote ya baba yako?”+ 21 Ndipo Sauli akasema: “Je, mimi si Mbenjamini kutoka katika kabila dogo zaidi kati ya makabila ya Israeli,+ na je, familia yangu si familia ya chini kabisa kati ya familia zote za kabila la Benjamini? Basi kwa nini unaniambia hivyo?”

22 Kisha Samweli akamchukua Sauli na mtumishi wake, akawaleta katika ukumbi wa kulia chakula, akawapa mahali pa kuketi mbele ya watu walioalikwa wapatao 30.⁠ 23 Samweli akamwambia mpishi: “Kilete chakula nilichokupa na kukuambia, ‘Kiweke kando.’” 24 Basi mpishi akainua ule mguu na nyama iliyokuwa juu yake, akauweka mbele ya Sauli. Samweli akasema: “Kilichokuwa kimehifadhiwa kimewekwa mbele yako. Kula, kwa maana kilihifadhiwa kwa ajili yako katika karamu hii. Kwa sababu niliwaambia, ‘Nimewaalika wageni.’” Basi Sauli akala pamoja na Samweli siku hiyo. 25 Kisha wakashuka kutoka mahali pa juu+ na kwenda jijini, naye akaendelea kuzungumza na Sauli kwenye paa la nyumba. 26 Wakaamka mapema, na kulipopambazuka, Samweli akamwita Sauli kutoka paani akisema: “Jitayarishe, ili nikusindikize.” Basi Sauli akajitayarisha na yeye pamoja na Samweli wakatoka nje. 27 Walipokuwa wakishuka kuelekea ukingoni mwa jiji, Samweli akamwambia Sauli: “Mwambie mtumishi+ atangulie mbele yetu,” basi akatangulia. “Lakini wewe, simama tuli sasa, ili nikujulishe neno la Mungu.”

10 Ndipo Samweli akachukua chupa ya mafuta na kuyamimina juu ya kichwa cha Sauli.+ Akambusu na kusema: “Yehova amekutia mafuta uwe kiongozi+ juu ya urithi wake.+ 2 Tutakapoachana leo, utakuta wanaume wawili karibu na kaburi la Raheli+ katika eneo la Benjamini kule Selsa, nao watakwambia, ‘Punda ulioenda kutafuta wamepatikana, lakini sasa baba yako amesahau kuhusu punda hao+ naye ana wasiwasi juu yako. Anauliza, “Nitafanya nini kuhusu mwanangu?”’ 3 Kutoka huko nenda mpaka kwenye mti mkubwa wa Tabori, na huko utakutana na wanaume watatu wakipanda kwenda kwa Mungu wa kweli kule Betheli,+ mmoja akiwa amebeba wanambuzi watatu, mwingine akiwa amebeba mikate mitatu, na mwingine akiwa amebeba mtungi mkubwa wa divai. 4 Watakusalimu na kukupa mikate miwili, unapaswa kuchukua mikate hiyo. 5 Kisha utafika kwenye kilima cha Mungu wa kweli, mahali ambapo pana kambi ya kijeshi ya Wafilisti. Utakapofika jijini, utakutana na kikundi cha manabii wakishuka kutoka mahali pa juu, na kinanda na tari na filimbi na kinubi vitapigwa mbele yao huku wakitoa unabii. 6 Roho ya Yehova itakutia nguvu,+ utatoa unabii pamoja nao, nawe utabadilishwa kuwa mtu tofauti.+ 7 Baada ya ishara hizo kutokea, fanya lolote unaloweza kufanya kwa mkono wako, kwa sababu Mungu wa kweli yuko pamoja nawe. 8 Kisha ushuke na kunitangulia kwenda Gilgali,+ nami nitakufuata huko ili nitoe dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ushirika. Unapaswa kungoja kwa siku saba mpaka nitakapofika. Halafu nitakujulisha jambo unalopaswa kufanya.”

9 Mara tu Sauli alipogeuka ili amwache Samweli, Mungu akaanza kuubadili moyo wake uwe kama wa mtu mwingine, na ishara hizo zote zikatimia siku hiyo. 10 Basi wakatoka hapo na kupanda kwenye kilima, na kikundi cha manabii kikakutana naye. Mara moja roho ya Mungu ikamtia nguvu,+ naye akaanza kutoa unabii+ kati yao. 11 Watu wote waliomjua awali walipomwona akitoa unabii pamoja na manabii, wakaulizana: “Mwana wa Kishi amepatwa na nini? Je, Sauli pia ni mmoja wa manabii?” 12 Ndipo mtu fulani wa mahali hapo akasema: “Lakini baba yao ni nani?” Basi kukawa na msemo* huu: “Je, Sauli pia ni mmoja wa manabii?”+

13 Alipomaliza kutoa unabii, akaenda mahali pa juu. 14 Baadaye ndugu ya baba ya Sauli akamuuliza Sauli na mtumishi wake: “Mlienda wapi?” Akajibu: “Kuwatafuta punda,+ lakini hatukuwapata, kwa hiyo tukaenda kwa Samweli.” 15 Ndugu ya baba ya Sauli akamuuliza: “Tafadhali niambie, Samweli alikuambia nini?” 16 Sauli akamjibu: “Alituambia kwamba tayari punda wamepatikana.” Lakini Sauli hakumwambia jambo ambalo Samweli alisema kuhusu ufalme.

17 Kisha Samweli akawaita watu ili wakusanyike mbele za Yehova huko Mispa,+ 18 akawaambia Waisraeli: “Yehova, Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Mimi ndiye niliyewatoa Waisraeli nchini Misri na kuwaokoa kutoka mikononi mwa Misri+ na kutoka mikononi mwa falme zote zilizokuwa zikiwakandamiza. 19 Lakini leo mmemkataa Mungu wenu+ aliyekuwa Mwokozi wenu aliyewaokoa kutoka katika maovu yenu yote na taabu zenu, nanyi mlisema: “Hatutaki, unapaswa kumweka mfalme atutawale.” Sasa simameni mbele za Yehova kulingana na makabila yenu na kulingana na maelfu yenu.’”*

20 Basi Samweli akaagiza makabila yote ya Israeli yakaribie,+ na kabila la Benjamini likachaguliwa.+ 21 Kisha akaagiza kabila la Benjamini likaribie kulingana na koo zao, basi ukoo wa Wamatri ukachaguliwa. Mwishowe Sauli mwana wa Kishi akachaguliwa.+ Lakini walipoenda kumtafuta, hawakumpata. 22 Kwa hiyo wakamuuliza Yehova:+ “Je, mtu huyo tayari amefika hapa?” Yehova akajibu: “Ndiye yule pale, amejificha kati ya mizigo.” 23 Basi wakakimbia na kumleta kutoka mahali hapo. Aliposimama katikati ya watu, alikuwa mrefu kuliko watu wote nao walimfikia mabegani.+ 24 Samweli akawaambia watu wote: “Je, mnamwona yule ambaye Yehova amemchagua,+ kwamba hakuna yeyote aliye kama yeye kati ya watu wote?” Basi watu wote wakaanza kupiga kelele wakisema: “Mfalme na aishi muda mrefu!”

25 Samweli akawaambia watu kuhusu haki za wafalme+ na kuziandika katika kitabu na kukiweka mbele za Yehova. Kisha Samweli akawaruhusu watu wote waende zao, kila mtu akaenda nyumbani kwake. 26 Sauli pia akaenda nyumbani kwake kule Gibea, akiwa pamoja na mashujaa ambao Yehova alikuwa amegusa mioyo yao. 27 Lakini wahuni fulani wakasema: “Huyu atatuokoaje?”+ Kwa hiyo wakamdharau, nao hawakumletea zawadi yoyote.+ Lakini hakusema jambo lolote kuhusu hilo.*

11 Nahashi Mwamoni+ akapanda na kupiga kambi ili kushambulia Yabeshi+ kule Gileadi. Watu wote wa Yabeshi wakamwambia Nahashi: “Fanya agano* pamoja nasi, nasi tutakutumikia.” 2 Nahashi Mwamoni akawaambia: “Nitafanya agano pamoja nanyi kwa sharti hili: macho yenu yote ya kulia yang’olewe. Nitafanya hivyo ili kuwaaibisha Waisraeli wote.” 3 Wazee wa Yabeshi wakamwambia: “Tupe muda wa siku saba ili tuwatume wajumbe katika eneo lote la Israeli. Na ikiwa hakuna yeyote wa kutuokoa, tutajisalimisha kwako.” 4 Baada ya muda, wajumbe hao wakafika katika jiji la Gibea+ la Sauli na kuwaambia watu wote maneno hayo, na watu wote wakalia kwa sauti kubwa sana.

5 Lakini Sauli alikuwa akitoka shambani akiwa nyuma ya mifugo yake, naye akauliza: “Watu wana shida gani? Kwa nini wanalia?” Basi wakamwambia maneno yaliyosemwa na watu wa Yabeshi. 6 Roho ya Mungu ikamtia nguvu Sauli+ alipoyasikia maneno hayo, akawaka hasira. 7 Kwa hiyo akachukua ng’ombe dume wawili, akawakata vipandevipande, akawatuma wajumbe wavipeleke katika eneo lote la Israeli wakisema: “Mtu yeyote ambaye hamfuati Sauli na Samweli ajue kwamba ng’ombe wake watafanyiwa hivi!” Na watu wakashikwa na hofu ya Yehova hivi kwamba wakatoka wote pamoja.* 8 Kisha akawahesabu kule Bezeki, Waisraeli walikuwa 300,000 na watu wa Yuda walikuwa 30,000. 9 Kwa hiyo wakawaambia wajumbe waliokuwa wamekuja: “Hivi ndivyo mnavyopaswa kuwaambia watu wa Yabeshi kule Gileadi, ‘Kesho wakati wa jua kali mtaokolewa.’” Basi wale wajumbe wakaja na kuwaambia watu wa Yabeshi, nao wakashangilia sana. 10 Ndipo watu wa Yabeshi wakasema: “Kesho tutajisalimisha kwenu, nanyi mtatutendea mpendavyo.”+

11 Siku iliyofuata, Sauli aliwagawa watu katika vikosi vitatu, nao wakaingia katikati ya kambi wakati wa kesha la alfajiri* na kuwaua Waamoni+ mpaka jua lilipokuwa kali. Watu waliookoka walitawanywa hivi kwamba hakuna watu wawili waliobaki pamoja. 12 Kisha watu wakamwambia Samweli: “Ni nani waliokuwa wakiuliza, ‘Je, Sauli atakuwa mfalme wetu?’+ Waleteni watu hao ili tuwaue.” 13 Hata hivyo, Sauli akasema: “Hakuna mtu yeyote anayepaswa kuuawa leo,+ kwa maana leo Yehova amewaokoa Waisraeli.”

14 Baadaye Samweli akawaambia watu: “Njooni twende Gilgali+ tukamtangaze tena mfalme.”+ 15 Basi watu wote wakaenda Gilgali, na huko Gilgali wakamweka Sauli kuwa mfalme mbele za Yehova. Kisha wakatoa huko dhabihu za ushirika mbele za Yehova,+ na Sauli na watu wote wa Israeli wakasherehekea kwa shangwe kubwa.+

12 Hatimaye Samweli akawaambia hivi Waisraeli wote: “Tazameni nimefanya* mambo yote mliyoomba nifanye, nami nimemweka mfalme awatawale.+ 2 Sasa huyu ndiye mfalme anayewaongoza ninyi!*+ Lakini mimi ni mzee mwenye mvi, na wanangu wako hapa pamoja nanyi,+ nami nimewaongoza tangu nilipokuwa kijana mpaka leo hii.+ 3 Niko mbele yenu. Toeni ushahidi dhidi yangu mbele za Yehova na mbele ya mtiwa-mafuta wake:+ Nimechukua ng’ombe dume wa nani au punda wa nani?+ Au nimemlaghai nani au kumkandamiza nani? Nimepokea rushwa kutoka kwa nani ili nipotoshe haki?*+ Ikiwa nimefanya hivyo, nitawarudishia.”+ 4 Nao wakasema: “Hujatulaghai wala kutukandamiza wala kupokea kitu chochote kile kutoka mkononi mwa yeyote.” 5 Basi akawaambia: “Yehova ni shahidi dhidi yenu, na mtiwa-mafuta wake ni shahidi leo kwamba hamkupata shtaka lolote dhidi yangu.”* Nao wakasema: “Yeye ni shahidi.”

6 Basi Samweli akawaambia watu: “Yehova, aliyemtumia Musa na Haruni na ambaye aliwatoa mababu zenu nchini Misri,+ ni shahidi. 7 Sasa simameni mahali penu, nami nitawahukumu mbele za Yehova kwa msingi wa matendo yote ya uadilifu ambayo Yehova amewatendea ninyi na mababu zenu.

8 “Baada tu ya Yakobo kuingia Misri+ na mababu zenu kuanza kumlilia Yehova awasaidie,+ Yehova alimtuma Musa+ na Haruni ili wawaongoze mababu zenu kutoka Misri na kuwawezesha kuishi mahali hapa.+ 9 Lakini walimsahau Yehova Mungu wao, naye akawauza+ mikononi mwa Sisera+ mkuu wa jeshi la Hasori na mikononi mwa Wafilisti+ na mikononi mwa mfalme wa Moabu,+ na maadui hao wakapigana nao. 10 Nao wakamlilia Yehova awasaidie+ na kusema, ‘Tumetenda dhambi,+ kwa maana tumekuacha wewe, Yehova, ili kuabudu Mabaali+ na sanamu za Ashtorethi;+ sasa tuokoe kutoka mikononi mwa maadui wetu ili tukutumikie.’ 11 Ndipo Yehova akamtuma Yerubaali+ na Bedani na Yeftha+ na Samweli,+ naye akawaokoa ninyi kutoka mikononi mwa maadui waliowazunguka, ili mwishi kwa usalama.+ 12 Mlipoona kwamba Nahashi,+ mfalme wa Waamoni amekuja kuwashambulia, mliniambia tena na tena, ‘Hatutaki, tumeazimia kuwa na mfalme wa kututawala!’+ hata ingawa Yehova Mungu wenu ndiye Mfalme wenu.+ 13 Sasa huyu ndiye mfalme mliyemchagua, mliyeomba. Tazameni! Yehova amemweka mfalme awatawale.+ 14 Mkimwogopa Yehova+ na kumtumikia+ na kuitii sauti yake+ na msipoasi agizo la Yehova, na ikiwa ninyi pamoja na mfalme anayewatawala mtamfuata Yehova Mungu wenu, itakuwa vyema. 15 Lakini msipotii sauti ya Yehova na mkiasi agizo la Yehova, mkono wa Yehova utawashambulia ninyi na baba zenu.+ 16 Sasa simameni mahali penu mwone jambo hili kubwa ambalo Yehova anatenda mbele ya macho yenu. 17 Je, huu si wakati wa kuvuna ngano? Nitamwomba Yehova alete ngurumo na mvua; ndipo mtakapojua na kuelewa uovu mkubwa mliofanya machoni pa Yehova kwa kuomba mfalme awatawale.”+

18 Basi Samweli akamwomba Yehova, naye Yehova akaleta ngurumo na mvua siku hiyo, hivi kwamba watu wote wakamwogopa sana Yehova na pia Samweli. 19 Na watu wote wakamwambia Samweli: “Sali kwa Yehova Mungu wako kwa ajili ya watumishi wako,+ kwa maana hatutaki kufa, kwa sababu tumeongeza uovu mwingine juu ya dhambi zetu zote kwa kuomba tupewe mfalme.”

20 Basi Samweli akawaambia watu: “Msiogope. Kwa kweli mmetenda uovu huu wote. Ila tu msigeuke na kuacha kumfuata Yehova,+ mtumikieni Yehova kwa moyo wenu wote.+ 21 Msigeuke na kufuata vitu vya ubatili,*+ ambavyo havina faida yoyote+ na ambavyo haviwezi kuokoa, kwa sababu ni vitu vya ubatili.* 22 Kwa ajili ya jina lake kuu,+ Yehova hatawaacha watu wake,+ kwa sababu Yehova ameamua mwenyewe kuwafanya ninyi kuwa watu wake.+ 23 Lakini mimi, siwezi kamwe kuwazia kumtendea Yehova dhambi kwa kuacha kusali kwa ajili yenu, nami nitaendelea kuwafundisha njia iliyo njema na iliyo sawa. 24 Ila tu mwogopeni Yehova,+ mtumikieni kwa uaminifu* kwa moyo wenu wote, kwa maana angalieni mambo makuu aliyowatendea.+ 25 Lakini mkifanya uovu bila kujali, ninyi pamoja na mfalme wenu mtafagiliwa mbali.”+

13 Sauli alikuwa na umri wa miaka . . .* alipowekwa kuwa mfalme,+ na kwa miaka miwili alitawala Israeli. 2 Sauli alichagua wanaume 3,000 katika Israeli; 2,000 kati yao walikuwa pamoja na Sauli kule Mikmashi na katika eneo lenye milima la Betheli, na 1,000 walikuwa pamoja na Yonathani+ katika jiji la Gibea+ la Benjamini. Aliwaruhusu waliobaki waende zao, kila mmoja kwenye hema lake. 3 Kisha Yonathani akaishambulia kambi ya kijeshi ya Wafilisti+ iliyokuwa Geba,+ na Wafilisti wakasikia habari hizo. Basi Sauli akaagiza pembe* ipigwe+ nchini kote, akisema: “Waebrania na wasikie!” 4 Waisraeli wote wakasikia habari hizi: “Sauli ameishambulia kambi ya kijeshi ya Wafilisti, na sasa Waisraeli wananuka mbele ya Wafilisti.” Basi watu wakakusanywa ili wamfuate Sauli huko Gilgali.+

5 Wafilisti pia wakakusanyika pamoja ili wapigane na Waisraeli, nao walikuwa na magari 30,000 ya vita na wapanda farasi 6,000 na wanajeshi wengi kama chembe za mchanga kwenye ufuo wa bahari;+ nao wakapanda na kupiga kambi kule Mikmashi upande wa mashariki wa Beth-aveni.+ 6 Na wanaume wa Israeli wakaona kwamba walikuwa hatarini, kwa sababu watu walikuwa chini ya mkazo mkali; basi watu wakajificha ndani ya mapango,+ mashimo, miamba, mahandaki, na hifadhi za maji. 7 Hata baadhi ya Waebrania walivuka Yordani na kuingia nchi ya Gadi na Gileadi.+ Lakini Sauli alikuwa bado Gilgali, na watu wote waliomfuata walikuwa wakitetemeka. 8 Aliendelea kungoja kwa siku saba mpaka wakati uliowekwa na Samweli ulipofika, lakini Samweli hakuja Gilgali, na watu walikuwa wakitawanyika kutoka kwake. 9 Mwishowe Sauli akasema: “Nileteeni dhabihu ya kuteketezwa na dhabihu za ushirika.” Basi akaitoa dhabihu ya kuteketezwa.+

10 Lakini mara tu alipomaliza kutoa dhabihu ya kuteketezwa, Samweli akafika. Kwa hiyo Sauli akaenda kumpokea na kumbariki. 11 Kisha Samweli akamuuliza: “Umefanya nini?” Sauli akamjibu: “Niliona kwamba watu wanatawanyika kutoka kwangu,+ nawe hukuja kwa wakati uliowekwa, na Wafilisti walikuwa wakikusanyika huko Mikmashi.+ 12 Kwa hiyo nikajiambia, ‘Sasa Wafilisti watashuka kunishambulia Gilgali, nami sijatafuta kibali cha* Yehova.’ Kwa hiyo nikahisi kwamba nina wajibu wa kutoa dhabihu ya kuteketezwa.”

13 Ndipo Samweli akamwambia Sauli: “Umetenda kipumbavu. Hukutii amri ambayo Yehova Mungu wako alikupa.+ Kama ungetii, Yehova angeimarisha ufalme wako juu ya Waisraeli milele. 14 Lakini sasa ufalme wako hautadumu.+ Yehova atamtafuta mtu anayeupendeza moyo wake,+ na Yehova atamweka kuwa kiongozi juu ya watu wake,+ kwa sababu hukutii mambo uliyoamriwa na Yehova.”+

15 Kisha Samweli akainuka na kupanda kwenda zake kutoka Gilgali mpaka jiji la Gibea la Benjamini, naye Sauli akawahesabu watu; wale waliobaki naye walikuwa wanaume wapatao 600.+ 16 Sauli na Yonathani mwana wake pamoja na watu waliobaki pamoja nao walikuwa wakikaa katika jiji la Geba+ la Benjamini, nao Wafilisti walikuwa wamepiga kambi kule Mikmashi.+ 17 Na makundi ya wavamizi yalikuwa yakitoka katika kambi ya Wafilisti katika vikosi vitatu. Kikosi kimoja kilikuwa kikielekea kwenye barabara inayoenda Ofra, katika nchi ya Shuali; 18 kikosi kingine kilikuwa kikielekea kwenye barabara ya Beth-horoni;+ na kikosi cha tatu kilikuwa kikifuata barabara inayoelekea kwenye mpaka ulio ng’ambo ya bonde la Seboimu, kuelekea nyikani.

19 Basi hakukuwa na fundi yeyote wa chuma katika nchi yote ya Israeli, kwa sababu Wafilisti walikuwa wamesema: “Ili Waebrania wasitengeneze upanga wala mkuki.” 20 Na Waisraeli wote walilazimika kushuka kwenda kwa Wafilisti ili majembe yao ya plau, sururu, mashoka, au miundu yao inolewe. 21 Bei ya kunoa ilikuwa pimu moja* kwa majembe ya plau, kwa sururu, kwa vifaa vyenye meno matatu, kwa mashoka, na pia kwa ajili ya kurekebisha mchokoo wa ng’ombe. 22 Na siku ya vita, hakuna yeyote kati ya watu waliokuwa pamoja na Sauli na Yonathani aliyekuwa na upanga wala mkuki mkononi mwake;+ Sauli na Yonathani mwanawe ndio tu waliokuwa na silaha.

23 Basi kikosi cha wanajeshi* Wafilisti kilikuwa kimeenda kwenye kivuko kilicho kwenye njia inayoenda Mikmashi.+

14 Siku moja Yonathani+ mwana wa Sauli alimwambia hivi mtumishi aliyembebea silaha: “Njoo tuvuke, twende kwenye kituo cha ulinzi cha Wafilisti upande wa pili.” Lakini hakumwambia baba yake jambo hilo. 2 Sauli alikuwa akikaa karibu na jiji la Gibea+ chini ya mkomamanga kule Migroni, na wanaume wapatao 600 walikuwa pamoja naye.+ 3 (Na Ahiya mwana wa Ahitubu,+ ndugu ya Ikabodi,+ mwana wa Finehasi,+ mwana wa Eli,+ kuhani wa Yehova kule Shilo,+ alikuwa amebeba efodi.)+ Na watu hawakujua kwamba Yonathani alikuwa ameondoka. 4 Basi kati ya njia ambazo Yonathani alijaribu kutumia kuvuka ili afike kwenye kituo cha ulinzi cha Wafilisti, kulikuwa na mwamba ulio na umbo la jino upande huu na mwamba mwingine ulio na umbo la jino upande wa pili; mwamba mmoja uliitwa Bosesi, na mwamba wa pili uliitwa Sene. 5 Mwamba mmoja ulikuwa nguzo upande wa kaskazini ng’ambo ya Mikmashi, na wa pili ulikuwa upande wa kusini ng’ambo ya Geba.+

6 Basi Yonathani akamwambia mtumishi wake aliyembebea silaha: “Njoo tuvuke na kwenda kwenye kituo cha ulinzi cha wanaume hawa wasiotahiriwa.+ Labda Yehova atatusaidia, kwa maana hakuna kitu chochote kinachoweza kumzuia Yehova kuokoa kwa kutumia watu wengi au wachache.”+ 7 Ndipo mtumishi wake aliyembebea silaha akamwambia: “Fanya jambo lolote ambalo moyo wako unakuchochea kufanya. Nenda popote unapotaka, nami nitakufuata popote ambapo moyo wako unakuchochea kwenda.” 8 Ndipo Yonathani akasema: “Tutavuka kwa wanaume wale ili watuone. 9 Wakituambia, ‘Simameni papo hapo mpaka tuje mlipo!’ basi tutasimama papo hapo, hatutapanda kwenda walipo. 10 Lakini wakisema, ‘Njooni hapa juu tupambane!’ tutapanda, kwa sababu Yehova atawatia mikononi mwetu. Hiyo ndiyo itakayokuwa ishara yetu.”+

11 Basi wote wawili wakajitokeza mbele ya kituo cha ulinzi cha Wafilisti. Wafilisti wakasema: “Tazameni! Waebrania wanatoka katika mashimo walimokuwa wamejificha.”+ 12 Kwa hiyo wanaume waliokuwa kwenye kituo hicho cha ulinzi wakamwambia Yonathani na mtumishi wake aliyembebea silaha: “Njooni hapa juu tulipo, nasi tutawafunza somo!”+ Mara moja Yonathani akamwambia hivi mtumishi aliyembebea silaha: “Nifuate, kwa kuwa Yehova atawatia mikononi mwa Waisraeli.”+ 13 Basi Yonathani akapanda kwa mikono na miguu yake, na mtumishi wake aliyembebea silaha alikuwa nyuma yake; na Yonathani akaanza kuwashambulia na kuwaangusha Wafilisti, na mtumishi wake aliyembebea silaha alikuwa akiwaua nyuma ya Yonathani. 14 Katika shambulizi la kwanza la Yonathani na mtumishi aliyembebea silaha, waliwaua wanaume wapatao 20 katika shamba lenye ukubwa wa karibu nusu eka linaloweza kulimwa kwa plau.*

15 Ndipo hofu ikaenea katika kambi iliyo shambani na miongoni mwa watu wote waliokuwa katika kituo cha ulinzi, na hata makundi ya wavamizi+ yakashikwa na hofu. Dunia ikaanza kutetemeka, kukawa na hofu kubwa kutoka kwa Mungu. 16 Walinzi wa Sauli waliokuwa katika jiji la Gibea+ la Benjamini wakaona kwamba machafuko yalikuwa yakienea kila upande.+

17 Sauli akawaambia watu waliokuwa pamoja naye: “Tafadhali, wahesabuni watu, mwone ni nani aliyetuacha.” Walipohesabu, wakagundua kwamba Yonathani na mtumishi wake aliyembebea silaha hawakuwepo. 18 Basi Sauli akamwambia Ahiya:+ “Lilete karibu Sanduku la Mungu wa kweli!” (Kwa maana wakati huo* Sanduku la Mungu wa kweli lilikuwa pamoja na Waisraeli.) 19 Sauli alipokuwa akiongea na kuhani, machafuko yaliyokuwa katika kambi ya Wafilisti yalizidi kuongezeka. Ndipo Sauli akamwambia hivi kuhani: “Acha unachofanya.”* 20 Kwa hiyo Sauli na watu wote waliokuwa pamoja naye wakakusanyika na kwenda vitani, na huko wakapata kwamba Wafilisti walikuwa wameshambuliana wenyewe kwa wenyewe kwa mapanga yao, na machafuko yalikuwa makubwa sana. 21 Pia, Waebrania ambao awali waliwaunga mkono Wafilisti na walioingia pamoja nao kambini walienda kujiunga na Waisraeli chini ya usimamizi wa Sauli na Yonathani. 22 Wanaume wote wa Israeli waliokuwa wamejificha+ katika eneo lenye milima la Efraimu wakasikia kwamba Wafilisti wamekimbia, nao pia wakaingia vitani na kuwafuatia. 23 Basi Yehova akawaokoa Waisraeli siku hiyo,+ na vita vikaenea mpaka Beth-aveni.+

24 Lakini wanaume wa Israeli walikuwa chini ya mkazo mkali siku hiyo, kwa kuwa Sauli alikuwa amewaapisha hivi: “Alaaniwe mtu yeyote atakayekula chakula chochote* kabla ya jioni na kabla sijalipiza kisasi dhidi ya maadui wangu!” Kwa hiyo hakuna yeyote miongoni mwao aliyekula chakula chochote.+

25 Basi watu wote wakafika* msituni, na kulikuwa na asali ardhini. 26 Watu walipoingia msituni, waliona asali ikidondoka, lakini hakuna yeyote aliyethubutu kunyoosha mkono wake ili kuila, kwa sababu waliogopa kile kiapo. 27 Lakini Yonathani hakumsikia baba yake akiwaapisha watu,+ kwa hiyo akanyoosha ncha ya fimbo iliyokuwa mkononi mwake na kuichovya ndani ya sega la asali. Alipourudisha mkono wake kinywani na kuila, macho yake yakang’aa. 28 Ndipo mtu mmoja akasema: “Baba yako aliwaapisha watu vikali akisema, ‘Na alaaniwe mtu atakayekula chakula leo!’+ Ndio sababu watu wamechoka sana.” 29 Hata hivyo, Yonathani akasema: “Baba yangu ameleta shida kubwa nchini. Angalieni jinsi macho yangu yalivyong’aa nilipoonja asali hii kidogo. 30 Hali ingekuwa bora zaidi ikiwa watu wangekula kwa uhuru+ leo baadhi ya nyara walizopata kutoka kwa maadui wao! Kwa maana Wafilisti wengi hata zaidi wangeuawa.”

31 Siku hiyo, waliendelea kuwaua Wafilisti kuanzia Mikmashi mpaka Aiyaloni,+ na watu wakachoka sana. 32 Basi watu wakaanza kukimbilia nyara kwa pupa, wakachukua kondoo na ng’ombe na ndama na kuwachinjia ardhini, nao wakala nyama pamoja na damu.+ 33 Basi Sauli akaambiwa hivi: “Tazama! Watu wanamtendea Yehova dhambi kwa kula nyama pamoja na damu.”+ Ndipo akasema: “Mmetenda kwa ukosefu wa imani. Bingirisheni jiwe kubwa juu yangu mara moja.” 34 Kisha Sauli akasema: “Nendeni kotekote miongoni mwa watu mkawaambie, ‘Ni lazima kila mmoja wenu aje na ng’ombe dume wake na kondoo wake mwachinjie hapa na kuwala. Msimtendee Yehova dhambi kwa kula nyama pamoja na damu.’”+ Basi kila mmoja wao akaja na ng’ombe dume wake usiku huo na kumchinjia mahali hapo. 35 Na Sauli akamjengea Yehova madhabahu.+ Hiyo ndiyo iliyokuwa madhabahu ya kwanza aliyomjengea Yehova.

36 Baadaye Sauli akasema: “Acheni tushuke tuwafuatie Wafilisti usiku na kuwapora mpaka asubuhi wakati wa mapambazuko. Hatutamwacha hai mtu yeyote.” Basi wakasema: “Fanya jambo lolote unaloona ni jema.” Kisha kuhani akasema: “Na tumkaribie Mungu wa kweli mahali hapa.”+ 37 Naye Sauli akamuuliza Mungu: “Je, nishuke nikawafuatie Wafilisti?+ Je, utawatia mikononi mwa Waisraeli?” Lakini Mungu hakumjibu siku hiyo. 38 Basi Sauli akasema: “Njooni hapa, enyi wakuu wote wa watu, mtafute ni dhambi gani iliyotendwa leo. 39 Kwa hakika kama anavyoishi Yehova, aliyewaokoa Waisraeli, hata kama ni mwanangu Yonathani, ni lazima afe.” Lakini hakuna mtu yeyote aliyemjibu. 40 Kisha akawaambia Waisraeli wote: “Mtakuwa upande mmoja, na mimi na mwanangu Yonathani tutakuwa upande wa pili.” Ndipo watu wakamwambia Sauli: “Fanya jambo lolote unaloona ni jema.”

41 Kisha Sauli akamwambia Yehova: “Ee Mungu wa Israeli, jibu kwa Thumimu!”+ Ndipo Yonathani na Sauli wakachaguliwa, nao watu wakawa huru. 42 Basi Sauli akasema: “Pigeni kura+ kuamua kati yangu na mwanangu Yonathani.” Kisha Yonathani akachaguliwa. 43 Halafu Sauli akamuuliza Yonathani: “Niambie, umefanya nini?” Yonathani akamwambia: “Nilionja tu asali kidogo kwa ncha ya fimbo iliyo mikononi mwangu.+ Nipo hapa! Niko tayari kufa!”

44 Basi Sauli akasema: “Mungu na akuadhibu, tena vikali, ikiwa hutakufa, Yonathani.”+ 45 Lakini watu wakamwambia Sauli: “Je, Yonathani afe, ambaye ameleta ushindi*+ huu mkubwa katika Israeli? Ni jambo lisiloweza kuwaziwa kamwe! Kwa hakika kama anavyoishi Yehova, hakuna unywele hata mmoja wa kichwa chake unaopaswa kuanguka ardhini, kwa maana alitenda pamoja na Mungu leo.”+ Hivyo watu wakamwokoa* Yonathani, naye hakufa.

46 Basi Sauli akaacha kuwafuatia Wafilisti, nao Wafilisti wakarudi katika eneo lao.

47 Sauli akauimarisha ufalme wake juu ya Waisraeli, akapigana na maadui wake wote waliomzunguka, alipigana na Wamoabu,+ Waamoni,+ Waedomu,+ wafalme wa Soba,+ na Wafilisti;+ na mahali popote alipoenda aliwashinda. 48 Alipigana kwa ushujaa na kuwashinda Waamaleki+ na kuwaokoa Waisraeli kutoka mikononi mwa waporaji.

49 Wana wa Sauli walikuwa Yonathani, Ishvi, na Malki-shua.+ Na alikuwa na mabinti wawili; mkubwa aliitwa Merabu,+ na mdogo aliitwa Mikali.+⁠ 50 Mke wa Sauli aliitwa Ahinoamu binti ya Ahimaazi. Mkuu wa jeshi lake aliitwa Abneri+ mwana wa Neri, ndugu ya baba ya Sauli. 51 Kishi+ alikuwa baba ya Sauli, na Neri+ baba ya Abneri alikuwa mwana wa Abieli.

52 Kulikuwa na vita vikali dhidi ya Wafilisti siku zote za Sauli.+ Sauli alipomwona mwanamume yeyote mwenye nguvu au jasiri alimwandikisha katika utumishi wake.+

15 Kisha Samweli akamwambia Sauli: “Yehova alinituma nikutie mafuta uwe mfalme juu ya watu wake Waisraeli,+ sasa sikiliza anavyosema Yehova.+ 2 Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Nitawaadhibu Waamaleki kwa sababu waliwapinga Waisraeli walipokuwa njiani wakipanda kutoka Misri.+ 3 Sasa, nenda uwashambulie Waamaleki+ na kuwaangamiza+ wao pamoja na vitu vyao vyote. Usiwaache hai;* unapaswa kuwaua,+ wanaume na wanawake, watoto wadogo na wale wanaonyonya, ng’ombe dume na kondoo, ngamia na pia punda.’”+ 4 Sauli akawakusanya watu na kuwahesabu huko Telaimu: Kulikuwa na wanajeshi 200,000 wanaotembea kwa miguu na wanaume 10,000 wa Yuda.+

5 Sauli akaenda mpaka kwenye jiji la Amaleki, akavizia kando ya bonde. 6 Ndipo Sauli akawaambia hivi Wakeni:+ “Nendeni, ondokeni kati ya Waamaleki ili nisiwafagilie mbali pamoja nao.+ Kwa maana mliwatendea watu wote wa Israeli+ kwa upendo mshikamanifu walipotoka Misri.” Basi Wakeni wakaondoka kati ya Waamaleki. 7 Kisha Sauli akawaangamiza Waamaleki+ kuanzia Havila+ mpaka Shuri,+ jiji lililo karibu na Misri. 8 Akamkamata Agagi+ mfalme wa Amaleki akiwa hai, lakini watu wengine wote akawaangamiza kwa upanga.+ 9 Hata hivyo, Sauli na watu wake walimwacha hai* Agagi na kondoo walio bora, ng’ombe, wanyama waliononeshwa, kondoo dume, na vitu vyote vizuri.+ Hawakutaka kuviangamiza. Lakini waliangamiza vitu vyote visivyo na thamani na visivyofaa.

10 Basi neno la Yehova likamjia Samweli: 11 “Ninasikitika* kwamba nimemweka Sauli kuwa mfalme, kwa sababu ameacha kunifuata naye hajatekeleza maneno yangu.”+ Samweli akakasirika sana, akaendelea kumlilia Yehova usiku kucha.+ 12 Samweli alipoamka asubuhi na mapema ili akutane na Sauli, aliambiwa hivi: “Sauli alienda Karmeli,+ na huko akajisimamishia mnara wa ukumbusho.+ Kisha akageuka na kushuka mpaka Gilgali.” 13 Mwishowe Samweli alipomfikia Sauli, Sauli akamwambia: “Yehova na akubariki. Nimetekeleza neno la Yehova.” 14 Lakini Samweli akamwambia: “Basi mbona nasikia milio ya kondoo na ng’ombe?”+ 15 Sauli akamjibu: “Waliletwa kutoka kwa Waamaleki, kwa sababu watu waliwaacha hai* kondoo bora na ng’ombe bora ili wawatoe dhabihu kwa Yehova Mungu wako; lakini vitu vilivyobaki tuliviangamiza.” 16 Ndipo Samweli akamwambia Sauli: “Nyamaza! Acha nikwambie jambo ambalo Yehova aliniambia jana usiku.”+ Basi akamwambia: “Sema!”

17 Samweli akamwambia: “Je, hukujiona kuwa mtu asiyefaa+ ulipowekwa kuwa kiongozi wa makabila ya Israeli na Yehova alipokutia mafuta kuwa mfalme wa Israeli?+ 18 Baadaye Yehova alikupa kazi na kukuambia, ‘Nenda, uwaangamize Waamaleki hao watenda dhambi.+ Pigana nao mpaka uwaangamize kabisa.’+ 19 Basi kwa nini hukuitii sauti ya Yehova? Badala yake, ulikimbilia nyara kwa pupa+ na kufanya maovu machoni pa Yehova!”

20 Hata hivyo, Sauli akamwambia Samweli: “Lakini nimeitii sauti ya Yehova! Nimefanya kazi ambayo Yehova alinituma nifanye, nikamleta Agagi mfalme wa Waamaleki na kuwaangamiza Waamaleki.+ 21 Lakini watu walichukua kondoo na ng’ombe kutoka kwenye nyara, vitu bora kati ya vitu vilivyopaswa kuangamizwa, ili wavitoe dhabihu kwa Yehova Mungu wako huko Gilgali.”+

22 Ndipo Samweli akasema: “Je, Yehova hupendezwa zaidi na dhabihu za kuteketezwa na dhabihu nyinginezo+ kuliko kuitii sauti ya Yehova? Tazama! Kutii ni bora kuliko dhabihu,+ na kusikiliza kuliko mafuta+ ya kondoo dume; 23 kwa maana uasi+ ni sawa na dhambi ya uaguzi,*+ na kutenda kwa kimbelembele ni sawa na kutumia nguvu za uchawi na ibada ya sanamu.* Kwa kuwa umelikataa neno la Yehova,+ yeye pia amekukataa usiwe mfalme.”+

24 Ndipo Sauli akamwambia Samweli: “Nimetenda dhambi, kwa kuwa nimeasi agizo la Yehova na maneno yako, kwa sababu niliwaogopa watu na kusikiliza maneno yao. 25 Sasa, tafadhali, nisamehe dhambi yangu, nawe urudi pamoja nami ili nimwinamie Yehova.”+ 26 Lakini Samweli akamwambia Sauli: “Sitarudi pamoja nawe, kwa kuwa umelikataa neno la Yehova, naye Yehova amekukataa usiendelee kuwa mfalme wa Israeli.”+ 27 Samweli alipokuwa akigeuka aende zake, Sauli akaushika upindo wa joho lake lisilo na mikono, lakini likararuka. 28 Ndipo Samweli akamwambia: “Yehova ameurarua ufalme wa Israeli kutoka kwako leo, naye atampa mwenzako aliye bora kuliko wewe.+ 29 Isitoshe, Mtukufu wa Israeli+ hatasema uwongo+ wala kubadili nia yake,* kwa maana Yeye si mwanadamu abadili nia yake.”*+

30 Sauli akasema: “Nimetenda dhambi. Lakini tafadhali niheshimu mbele ya wazee wa watu wangu na mbele ya Waisraeli. Rudi pamoja nami, nami nitamwinamia Yehova Mungu wako.”+ 31 Basi Samweli akarudi pamoja na Sauli, na Sauli akamwinamia Yehova. 32 Kisha Samweli akasema: “Mleteni hapa Agagi mfalme wa Waamaleki.” Ndipo Agagi akaja kwake akisitasita,* kwa sababu Agagi alisema moyoni mwake: “Kwa hakika hatari ya kifo imepita.”* 33 Hata hivyo, Samweli akasema: “Kama upanga wako ulivyofanya wanawake wafiwe na watoto, ndivyo mama yako atakavyofiwa zaidi miongoni mwa wanawake.” Papo hapo Samweli akamkatakata Agagi vipandevipande mbele za Yehova huko Gilgali.+

34 Kisha Samweli akaenda zake Rama, naye Sauli akapanda kwenda nyumbani kwake katika jiji la Gibea la Sauli. 35 Samweli hakumwona Sauli tena mpaka siku alipokufa, kwa maana Samweli alikuwa akimwombolezea Sauli.+ Yehova akaghairi kwamba alikuwa amemweka Sauli kuwa mfalme wa Israeli.+

16 Mwishowe Yehova akamuuliza Samweli: “Kwa kuwa nimemkataa Sauli asitawale akiwa mfalme wa Israeli,+ utaendelea kumwombolezea mpaka lini?+ Jaza pembe yako mafuta,+ uende. Nitakutuma kwa Yese+ Mbethlehemu, kwa sababu nimejichagulia mfalme kutoka miongoni mwa wanawe.”+ 2 Lakini Samweli akasema: “Nitaendaje? Sauli akisikia habari hii, ataniua.”+ Yehova akamwambia: “Nenda na ng’ombe mchanga, useme, ‘Nimekuja kumtolea Yehova dhabihu.’ 3 Mwalike Yese kwenye dhabihu; kisha nitakujulisha utakalofanya. Utamtia mafuta kwa ajili yangu yule nitakayekuonyesha.”+

4 Samweli alifanya mambo aliyoambiwa na Yehova. Alipofika Bethlehemu,+ wazee wa jiji walitetemeka walipokutana naye, wakamuuliza: “Je, umekuja kwa amani?” 5 Akajibu: “Nimekuja kwa amani. Nimekuja kumtolea Yehova dhabihu. Jitakaseni, mje pamoja nami kwenye dhabihu.” Kisha akamtakasa Yese na wanawe, halafu akawaalika kwenye dhabihu. 6 Walipokuwa wakiingia, Samweli alimwona Eliabu+ na kusema: “Hakika mtiwa-mafuta wa Yehova amesimama hapa mbele zake.” 7 Lakini Yehova akamwambia Samweli: “Usitazame sura yake wala urefu wake,+ kwa maana nimemkataa. Kwa kuwa Mungu haoni kama mwanadamu anavyoona, kwa maana mwanadamu huona kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona ndani ya moyo.”+ 8 Kisha Yese akamwita Abinadabu,+ akampitisha mbele ya Samweli, lakini Samweli akasema: “Huyu pia Yehova hajamchagua.” 9 Kisha Yese akampitisha Shamma,+ lakini Samweli akasema: “Hata huyu Yehova hajamchagua.” 10 Basi Yese akawapitisha wanawe saba mbele ya Samweli, lakini Samweli akamwambia Yese: “Yehova hajamchagua yeyote kati ya hawa.”

11 Mwishowe Samweli akamuuliza Yese: “Je, hawa ndio wana wako wote?” Akajibu: “Aliye mdogo zaidi+ ameachwa mpaka sasa; anawalisha kondoo.”+ Kisha Samweli akamwambia Yese: “Mtume mtu akamwite, kwa sababu hatutaketi kula chakula mpaka atakapokuja hapa.” 12 Basi akamtuma mtu amwite, Yese akamleta ndani. Kijana huyo alikuwa mwekundu, mwenye macho yanayovutia, na mwenye sura nzuri.+ Ndipo Yehova akasema: “Simama, mtie mafuta, kwa maana huyu ndiye!”+ 13 Basi Samweli akachukua ile pembe ya mafuta+ na kumtia mafuta mbele ya ndugu zake. Na roho ya Yehova ikaanza kumtia nguvu Daudi kuanzia siku hiyo na kuendelea.+ Baadaye Samweli akainuka na kwenda zake Rama.+

14 Sasa roho ya Yehova ilikuwa imemwacha Sauli,+ na roho mbaya kutoka kwa Yehova ilikuwa ikimtesa.+ 15 Watumishi wa Sauli wakamwambia: “Unaona kwamba roho mbaya kutoka kwa Mungu inakutesa. 16 Tafadhali, bwana wetu, waamuru watumishi wako walio mbele yako wamtafute mtu mwenye ustadi wa kupiga kinubi.+ Wakati wowote roho mbaya kutoka kwa Mungu inapokujia, atapiga kinubi, nawe utahisi vizuri.” 17 Basi Sauli akawaambia watumishi wake: “Tafadhali, nitafutieni mtu anayepiga kinubi vizuri, mumlete kwangu.”

18 Mtumishi mmoja akasema: “Tazama! Nimeona mwana fulani wa Yese Mbethlehemu anavyopiga kinubi kwa ustadi, ni mtu jasiri na shujaa hodari.+ Ana ustadi wa kuongea, ana sura nzuri,+ na Yehova yuko pamoja naye.”+ 19 Ndipo Sauli akawatuma wajumbe kwa Yese na kumwambia: “Mtume mwana wako Daudi aje kwangu, yule anayechunga kondoo.”+ 20 Basi Yese akapakia mikate, kiriba cha ngozi chenye divai, na mwanambuzi juu ya punda, akamtuma Daudi mwana wake kwa Sauli akiwa na vitu hivyo. 21 Kwa hiyo Daudi akafika kwa Sauli na kuanza kumtumikia.+ Sauli akampenda sana, naye Daudi akawa akimbebea silaha zake. 22 Sauli akamtumia Yese ujumbe huu: “Tafadhali, mruhusu Daudi aendelee kunitumikia, kwa sababu amepata kibali machoni pangu.” 23 Wakati wowote roho mbaya kutoka kwa Mungu ilipomjia Sauli, Daudi alichukua kinubi na kukipiga, kisha Sauli alipata kitulizo na kuhisi vizuri, na roho hiyo mbaya ilimwacha.+

17 Sasa Wafilisti+ wakakusanya majeshi yao* kwa ajili ya vita. Walikusanyika huko Soko,+ jiji la Yuda, wakapiga kambi kati ya Soko na Azeka,+ kule Efes-damimu.+ 2 Sauli na wanaume wa Israeli wakakusanyika na kupiga kambi katika Bonde la* Ela,+ nao wakajipanga kivita ili kupigana na Wafilisti. 3 Wafilisti walikuwa upande mmoja wa mlima, na Waisraeli walikuwa upande ule mwingine, na bonde lilikuwa katikati yao.

4 Kisha shujaa mmoja akatoka katika kambi za Wafilisti; aliitwa Goliathi,+ kutoka Gathi,+ alikuwa na urefu wa mikono sita na shubiri moja.* 5 Alikuwa na kofia ya shaba kichwani, naye alivaa koti la vita lenye magamba yanayolaliana. Koti hilo la vita la shaba+ lilikuwa na uzito wa shekeli 5,000.* 6 Alikuwa na mabamba ya shaba yaliyokinga miguu yake na fumo+ la shaba lililoning’inia katikati ya mabega yake. 7 Mpini wa mbao wa mkuki wake ulikuwa kama mti wa wafumaji wa nguo,+ na kichwa cha chuma cha mkuki wake kilikuwa na uzito wa shekeli 600;* na mtu aliyembebea ngao alitembea mbele yake. 8 Basi akasimama na kuviita vikosi vya Israeli+ akisema: “Kwa nini mmekuja kujipanga kivita? Je, mimi si Mfilisti nanyi je, si watumishi wa Sauli? Jichagulieni mwanamume, aje kupigana nami. 9 Akiweza kupigana nami na kuniua, tutakuwa watumishi wenu. Lakini nikimshinda na kumuua, mtakuwa watumishi wetu, nanyi mtatutumikia.” 10 Kisha Mfilisti huyo akasema: “Ninavitukana* vikosi vya Israeli+ leo. Nipeni mwanamume, nipigane naye!”

11 Sauli na Waisraeli wote waliposikia maneno hayo ya Mfilisti huyo, wakashikwa na hofu na kuogopa sana.

12 Basi Daudi alikuwa mwana wa Yese,+ Mwefrathi+ kutoka mji wa Bethlehemu+ wa Yuda, ambaye alikuwa na wana wanane+ na ambaye katika siku za Sauli alikuwa tayari amezeeka. 13 Wana watatu wakubwa wa Yese walikuwa wameenda na Sauli vitani.+ Majina ya wana hao watatu walioenda vitani ni Eliabu+ mzaliwa wake wa kwanza, Abinadabu+ mwana wake wa pili, na Shamma mwana wake wa tatu.+ 14 Daudi ndiye aliyekuwa mdogo zaidi,+ na wale watatu wakubwa walikuwa wameenda pamoja na Sauli.

15 Daudi alikuwa akienda na kurudi kutoka kwa Sauli ili kuchunga kondoo+ wa baba yake huko Bethlehemu. 16 Wakati huo, yule Mfilisti alikuwa akija na kuwadhihaki kila asubuhi na kila jioni kwa siku 40.

17 Ndipo Yese akamwambia Daudi mwana wake: “Tafadhali, chukua hii efa* ya nafaka iliyokaangwa na mikate hii kumi, uwapelekee haraka ndugu zako kambini. 18 Nawe umpelekee mkuu wa elfu mafungu haya kumi ya jibini;* pia, angalia ndugu zako wanaendeleaje na uniletee kitu fulani kutoka kwao.” 19 Walikuwa pamoja na Sauli na wanaume wengine wote wa Israeli katika Bonde la* Ela,+ wakipigana na Wafilisti.+

20 Kwa hiyo Daudi akaamka asubuhi na mapema na kuwaacha kondoo mikononi mwa mtu mwingine; kisha akapakia vitu hivyo na kwenda kama Yese alivyokuwa amemwamuru. Alipofika kambini, jeshi lilikuwa likienda kwenye uwanja wa vita huku likipiga kelele za vita. 21 Waisraeli na Wafilisti wakajipanga kivita wakikabiliana uso kwa uso. 22 Mara moja Daudi akaiacha mizigo yake mikononi mwa mtu aliyetunza mizigo, akakimbia kwenda kwenye uwanja wa vita. Alipofika, akaanza kuulizia habari za ndugu zake.+

23 Alipokuwa akizungumza nao, akaja yule Mfilisti shujaa aliyeitwa Goliathi,+ kutoka Gathi. Alitoka katika vikosi vya Wafilisti, akasema maneno yaleyale aliyozoea kusema,+ na Daudi akamsikia. 24 Wanaume wote wa Israeli walipomwona mwanamume huyo, wakaogopa sana na kumkimbia.+ 25 Wanaume wa Israeli walikuwa wakisema: “Je, mnamwona mwanamume yule anayekuja? Anakuja kuwatukana* Waisraeli.+ Mfalme atampa utajiri mwingi mtu atakayemuua mwanamume huyo, atampa pia binti yake mwenyewe,+ naye ataiondolea wajibu nyumba ya baba yake katika Israeli.”

26 Daudi akaanza kuwauliza wanaume waliokuwa wamesimama karibu naye: “Mtu atakayemuua yule Mfilisti na kuwaondolea Waisraeli aibu atafanyiwa nini? Kwani huyu Mfilisti asiyetahiriwa ni nani hata avitukane* vikosi vya Mungu aliye hai?”+ 27 Basi watu hao wakamwambia maneno yaleyale yaliyokuwa yamesemwa: “Hivi ndivyo atakavyofanyiwa mwanamume atakayemuua.” 28 Eliabu ndugu yake mkubwa+ alipomsikia Daudi akizungumza na wanaume hao, akamkasirikia Daudi na kumwambia: “Kwa nini umeshuka huku? Na wale kondoo wachache nyikani umemwachia nani?+ Najua vizuri kimbelembele chako na nia mbaya ya moyo wako; umeshuka tu ili kutazama vita.” 29 Daudi akamwambia: “Sasa nimefanya nini? Nilikuwa nikiuliza swali tu!” 30 Ndipo Daudi akamwacha, akamgeukia mtu mwingine na kumuuliza swali lilelile,+ na watu wakamjibu vilevile kama mwanzoni.+

31 Watu wakasikia maneno aliyosema Daudi, wakamwambia Sauli. Basi Sauli akaagiza aitwe. 32 Daudi akamwambia Sauli: “Mtu yeyote asife moyo* kwa sababu yake. Mimi mtumishi wako nitaenda kupigana na huyo Mfilisti.”+ 33 Lakini Sauli akamwambia Daudi: “Huwezi kwenda kupigana na huyo Mfilisti, kwa sababu wewe ni mvulana tu,+ naye amekuwa mwanajeshi* tangu alipokuwa kijana.” 34 Ndipo Daudi akamwambia Sauli: “Mimi mtumishi wako nimekuwa nikichunga kondoo wa baba yangu, na simba+ akaja, na pia dubu, na kila mmoja wao akamchukua kondoo kutoka kundini. 35 Nilimfuata, nikamuua na kumwokoa kondoo kutoka kinywani mwake. Aliporuka ili kunishambulia, nilimkamata manyoya yake,* nikampiga, na kumuua. 36 Mimi mtumishi wako nilimuua simba na dubu pia, na huyu Mfilisti asiyetahiriwa atakuwa kama mmoja wao, kwa sababu amevitukana* vikosi vya Mungu aliye hai.”+ 37 Kisha Daudi akasema: “Yehova, aliyeniokoa kutoka katika makucha ya simba na ya dubu, ndiye atakayeniokoa kutoka mikononi mwa Mfilisti huyo.”+ Ndipo Sauli akamwambia Daudi: “Nenda, na Yehova awe pamoja nawe.”

38 Basi Sauli akamvisha Daudi mavazi yake. Akamvisha kofia ya shaba kichwani, halafu akamvisha koti la vita. 39 Kisha Daudi akajifunga upanga wake juu ya mavazi yake, akajaribu kutembea lakini akashindwa kwa sababu hakuwa ameyazoea. Basi Daudi akamwambia Sauli: “Siwezi kwenda nikiwa nimevaa vitu hivi, kwa maana sijavizoea.” Kwa hiyo Daudi akavivua. 40 Kisha akachukua fimbo yake mkononi, akajichagulia mawe matano laini kutoka katika bonde la kijito, akayaweka kwenye kifuko ndani ya mfuko wake wa mchungaji, na kombeo+ lilikuwa mkononi mwake. Naye akaanza kumkaribia huyo Mfilisti.

41 Mfilisti huyo akaanza kumkaribia Daudi zaidi na zaidi, na mtu aliyembebea ngao alikuwa mbele yake. 42 Mfilisti huyo alipotazama na kumwona Daudi, akaanza kumdhihaki kwa dharau kwa sababu alikuwa tu mvulana mwekundu mwenye sura nzuri.+ 43 Basi Mfilisti huyo akamuuliza Daudi: “Je, mimi ni mbwa+ hivi kwamba unijie na vijiti?” Ndipo huyo Mfilisti akamlaani Daudi kwa miungu yake. 44 Akamwambia Daudi: “Nikaribie tu, nyama yako nitawapa ndege wa angani na wanyama wa mwituni.”

45 Daudi akamjibu hivi huyo Mfilisti: “Unakuja kupigana nami kwa upanga, mkuki, na fumo,+ lakini mimi naja kupigana nawe kwa jina la Yehova wa majeshi,+ Mungu wa vikosi vya Israeli, ambaye umemtukana.*+ 46 Siku hii ya leo Yehova atakutia wewe mikononi mwangu,+ nami nitakuua na kukata kichwa chako; na siku ya leo nitawapa ndege wa angani na wanyama mwitu wa dunia maiti za kambi ya Wafilisti; na watu wote duniani watajua kwamba kuna Mungu katika Israeli.+ 47 Na watu wote waliokusanyika hapa watajua* kwamba Yehova haokoi kwa upanga wala kwa mkuki,+ kwa sababu vita ni vya Yehova,+ naye atawatia ninyi nyote mikononi mwetu.”+

48 Basi Mfilisti huyo akasimama, akazidi kukaribia ili akutane na Daudi, lakini Daudi akakimbia haraka kuelekea kwenye uwanja wa vita kukutana na Mfilisti huyo. 49 Daudi akautia mkono wake ndani ya mfuko wake, akachukua jiwe kutoka humo, na kulirusha kwa kombeo. Akampiga Mfilisti huyo kwenye paji la uso, na jiwe hilo likapenya katika paji la uso wake, akaanguka chini kifudifudi.+ 50 Basi Daudi akamshinda Mfilisti huyo kwa kombeo na jiwe; alimpiga Mfilisti huyo na kumuua, ingawa Daudi hakuwa na upanga mkononi mwake.+ 51 Daudi akaendelea kukimbia na kusimama juu yake. Kisha akaushika upanga wa Mfilisti+ huyo na kuuchomoa kutoka katika ala yake, akahakikisha kwamba amekufa kwa kumkata kichwa kwa upanga huo. Wafilisti walipoona kwamba shujaa wao amekufa, wakakimbia.+

52 Kisha wanaume wa Israeli na Yuda wakainuka na kuanza kupiga kelele na kuwafuatia Wafilisti kuanzia bondeni+ mpaka kwenye malango ya Ekroni,+ na maiti za Wafilisti waliouawa zilienea barabarani kuanzia Shaaraimu,+ mpaka Gathi na Ekroni. 53 Waisraeli waliporudi baada ya kuwafuatia vikali Wafilisti, walipora kambi zao.

54 Halafu Daudi akachukua kichwa cha yule Mfilisti na kukileta Yerusalemu, lakini akaziweka silaha za Mfilisti huyo ndani ya hema lake mwenyewe.+

55 Sauli alipomwona Daudi akienda kupigana na Mfilisti huyo, alimuuliza hivi Abneri+ mkuu wa jeshi: “Abneri, mvulana huyu ni mwana wa nani?”+ Abneri akajibu: “Kwa hakika kama unavyoishi,* Ee mfalme, mimi sijui!” 56 Mfalme akasema: “Tafuta mvulana huyu ni mwana wa nani.” 57 Basi mara tu Daudi aliporudi baada ya kumuua huyo Mfilisti, Abneri akamchukua na kumpeleka mbele ya Sauli akiwa na kichwa cha huyo Mfilisti+ mkononi mwake. 58 Ndipo Sauli akamuuliza: “Mvulana, wewe ni mwana wa nani?” Daudi akamjibu: “Mimi ni mwana wa mtumishi wako Yese+ Mbethlehemu.”+

18 Baada tu ya Daudi kumaliza kuzungumza na Sauli, Yonathani+ na Daudi wakashikamana na kuwa marafiki wa karibu sana,* na Yonathani akaanza kumpenda kama alivyojipenda mwenyewe.*+ 2 Kuanzia siku hiyo, Sauli akamchukua Daudi, naye hakumruhusu arudi nyumbani kwa baba yake.+ 3 Na Yonathani na Daudi wakafanya agano,+ kwa sababu alimpenda kama alivyojipenda mwenyewe.*+ 4 Yonathani akavua joho lake lisilo na mikono na kumpa Daudi, pamoja na silaha zake, upanga wake, upinde wake, na mshipi wake. 5 Daudi akaanza kwenda vitani, naye alifanikiwa*+ popote alipotumwa na Sauli. Basi Sauli akamweka asimamie wanajeshi vitani,+ na jambo hilo likawafurahisha watu wote na pia watumishi wa Sauli.

6 Daudi na watu wengine walipokuwa wakirudi baada ya kuwaua Wafilisti, wanawake walikuwa wakitoka katika majiji yote ya Israeli wakiimba+ na kucheza dansi ili kumpokea Mfalme Sauli kwa matari,+ kwa vigelegele, na udi. 7 Wanawake hao waliokuwa wakisherehekea walikuwa wakiimba hivi:

“Sauli ameua maelfu yake,

Na Daudi makumi yake ya maelfu.”+

8 Sauli akakasirika sana,+ na wimbo huo haukumpendeza kwa kuwa alisema: “Wamempa Daudi makumi ya maelfu, lakini mimi wamenipa maelfu. Lililobaki tu ni kumpa ufalme!”+ 9 Kuanzia siku hiyo na kuendelea, Sauli alikuwa akimtilia shaka Daudi.

10 Siku iliyofuata, roho mbaya kutoka kwa Mungu ikamvamia Sauli,+ naye akaanza kutenda kwa njia ya ajabu* nyumbani, huku Daudi akipiga muziki kwa kinubi+ kama alivyofanya nyakati nyingine. Sauli alikuwa na mkuki mkononi,+ 11 basi akaurusha mkuki huo+ akisema hivi moyoni: ‘Nitampigilia Daudi ukutani!’ Lakini Daudi alimkwepa mara mbili. 12 Ndipo Sauli akamwogopa Daudi kwa sababu Yehova alikuwa pamoja naye+ lakini alikuwa amemwacha yeye.*+ 13 Kwa hiyo Sauli akamwondoa nyumbani mwake na kumweka kuwa mkuu wa elfu, basi Daudi alikuwa akiliongoza jeshi vitani.*+ 14 Daudi akaendelea kufanikiwa*+ katika mambo yote aliyofanya, na Yehova alikuwa pamoja naye.+ 15 Sauli alipoona kwamba Daudi anafanikiwa sana, akaanza kumwogopa. 16 Lakini watu wote wa Israeli na Yuda walimpenda Daudi, kwa sababu alikuwa akiwaongoza vitani.

17 Baadaye Sauli akamwambia Daudi: “Ndiye huyu Merabu binti yangu mkubwa.+ Nitakupa awe mke wako.+ Lakini unapaswa kuendelea kunitumikia kwa ujasiri na kupigana vita vya Yehova.”+ Kwa maana Sauli alisema hivi moyoni: ‘Mkono wangu usimuue. Acha mikono ya Wafilisti imuue.’+ 18 Ndipo Daudi akamwambia Sauli: “Mimi ni nani na watu wangu wa ukoo ni nani, au familia ya baba yangu katika Israeli, hata mfalme awe baba mkwe wangu?”+ 19 Hata hivyo, wakati ulipofika wa kumpa Daudi Merabu, binti ya Sauli, tayari Adrieli+ Mmeholathi alikuwa amepewa binti huyo awe mke wake.

20 Sasa Mikali+ binti ya Sauli alimpenda Daudi, Sauli akajulishwa jambo hilo, nalo likampendeza. 21 Kwa hiyo Sauli akasema: “Nitampa Daudi binti huyo ili awe mtego kwake, na ili mikono ya Wafilisti imuue.”+ Kisha Sauli akamwambia hivi Daudi mara ya pili: “Utafanya mapatano ya ndoa pamoja nami* leo.” 22 Pia, Sauli akawaamuru hivi watumishi wake: “Zungumzeni na Daudi kwa siri na kumwambia, ‘Tazama! Mfalme anakupenda, na watumishi wake wote wanakupenda sana. Basi sasa fanya mapatano ya ndoa na mfalme.’” 23 Watumishi wa Sauli walipomwambia Daudi mambo hayo, Daudi akasema: “Je, mnafikiri ni jambo rahisi kwa mtu maskini na asiyeheshimiwa sana kama mimi kufanya mapatano ya ndoa na mfalme?”+ 24 Kisha watumishi wa Sauli wakamletea habari hii: “Haya ndiyo maneno aliyosema Daudi.”

25 Kwa hiyo Sauli akasema: “Hivi ndivyo mnavyopaswa kumwambia Daudi: ‘Mfalme hataki mahari yoyote+ isipokuwa magovi 100 ya Wafilisti,+ ili mfalme awalipize kisasi maadui wake.’” Lakini Sauli alikuwa anapanga njama ili Wafilisti wamuue Daudi. 26 Basi watumishi wake wakamwambia Daudi habari hiyo, na habari hiyo ya kufanya mapatano ya ndoa na mfalme ikampendeza Daudi.+ Kabla ya siku iliyopangwa kufika, 27 Daudi alienda na wanaume wake na kuwaua wanaume 200 Wafilisti, na Daudi akamletea mfalme idadi kamili ya magovi yao, ili afanye mapatano ya ndoa na mfalme. Basi Sauli akampa Daudi Mikali binti yake awe mke wake.+ 28 Sauli akatambua kwamba Yehova alikuwa pamoja na Daudi+ na Mikali binti yake alimpenda Daudi.+ 29 Jambo hilo likamfanya Sauli azidi kumwogopa Daudi, basi Sauli akawa adui ya Daudi maisha yake yote.+

30 Watawala wa Wafilisti walikuwa wakienda vitani, lakini kadiri walivyoenda, ndivyo Daudi alivyozidi kufanikiwa* kuliko watumishi wote wa Sauli;+ na jina lake liliheshimiwa sana.+

19 Baadaye Sauli akazungumza na Yonathani mwana wake na watumishi wake wote kuhusu kumuua Daudi.+ 2 Kwa kuwa Yonathani mwana wa Sauli alimpenda sana Daudi,+ alimwambia hivi Daudi: “Sauli baba yangu anakusudia kukuua. Tafadhali jihadhari itakapofika asubuhi, nenda mahali pa siri na ujifiche huko. 3 Nitakuja na kusimama kando ya baba yangu shambani mahali utakapokuwa. Nitaongea na baba yangu kukuhusu, nikipata habari yoyote, bila shaka nitakuambia.”+

4 Basi Yonathani akamsifu Daudi+ mbele ya Sauli baba yake. Akamwambia: “Mfalme, usimtendee dhambi mtumishi wako Daudi kwa sababu yeye hajakutendea dhambi na mambo aliyokufanyia yamekunufaisha. 5 Alihatarisha uhai wake* alipomuua yule Mfilisti,+ na Yehova akawapa Waisraeli wote ushindi* mkubwa. Uliona jambo hilo, ukashangilia sana. Basi kwa nini uitendee dhambi damu isiyo na hatia kwa kuagiza Daudi auawe bila sababu?”+ 6 Sauli akamsikiliza Yonathani na kuapa hivi: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, hatauawa.” 7 Baadaye Yonathani akamwita Daudi na kumwambia mambo hayo yote. Kisha Yonathani akampeleka Daudi kwa Sauli, naye akaendelea kumtumikia kama awali.+

8 Baada ya muda vita vikatokea tena, na Daudi akaenda kupigana na Wafilisti na kuwaua Wafilisti wengi sana, nao wakakimbia kutoka mbele yake.

9 Na roho mbaya kutoka kwa Yehova ikamjia Sauli+ alipokuwa ameketi nyumbani mwake akiwa na mkuki mkononi, huku Daudi akipiga muziki kwa kinubi.+ 10 Sauli akajaribu kumpigilia Daudi ukutani kwa mkuki, lakini akamkwepa Sauli, na mkuki huo ukapenya ukutani. Daudi akakimbia na kutoroka usiku huo. 11 Baadaye Sauli akawatuma wajumbe nyumbani kwa Daudi ili wailinde na kumuua asubuhi,+ lakini Mikali mke wa Daudi akamwambia Daudi: “Usipotoroka usiku wa leo, kesho utakuwa mfu.” 12 Mara moja Mikali akamteremsha Daudi kupitia dirishani, ili akimbie na kutoroka. 13 Mikali akachukua sanamu ya terafimu* na kuiweka kitandani, akaifunika kwa vazi na kuweka wavu wa manyoya ya mbuzi mahali ambapo Daudi hulaza kichwa chake.

14 Basi Sauli akawatuma wajumbe wamlete Daudi, lakini mke wa Daudi akawaambia: “Ni mgonjwa.” 15 Kisha Sauli akawatuma wajumbe hao wamwone Daudi, akawaambia: “Mleteni kwangu akiwa kwenye kitanda chake ili auawe.”+ 16 Wajumbe hao walipoingia, walikuta sanamu ya terafimu* kitandani na wavu wa manyoya ya mbuzi mahali anapolaza kichwa chake. 17 Sauli akamuuliza Mikali: “Kwa nini ulinidanganya hivi na kumwacha adui yangu+ akimbie na kutoroka?” Mikali akamjibu Sauli: “Aliniambia, ‘Niache niende, nisije nikakuua!’”

18 Basi Daudi alikimbia na kutoroka, akafika kwa Samweli kule Rama.+ Akamwambia mambo yote ambayo Sauli alikuwa amemtendea. Kisha yeye na Samweli wakaenda zao, wakakaa kule Naiothi.+ 19 Baada ya muda Sauli aliambiwa hivi: “Tazama! Daudi yuko Naiothi kule Rama.” 20 Mara moja Sauli akawatuma wajumbe wamkamate Daudi. Walipowaona manabii waliozeeka wakitoa unabii na Samweli akiwa amesimama na kuwaongoza, roho ya Mungu ikawajia wajumbe wa Sauli, nao pia wakaanza kutenda kama manabii.

21 Walipomwambia Sauli habari hizo, mara moja akawatuma wajumbe wengine, nao pia wakaanza kutenda kama manabii. Basi Sauli akawatuma tena wajumbe wengine, kikundi cha tatu, nao pia wakaanza kutenda kama manabii. 22 Mwishowe yeye pia akaenda Rama. Alipofika kwenye tangi kubwa la maji lililoko Seku, akauliza: “Samweli na Daudi wako wapi?” Wakamjibu: “Wako Naiothi+ kule Rama.” 23 Sauli alipokuwa njiani kutoka huko kwenda Naiothi kule Rama, roho ya Mungu ikamjia pia, naye akatembea huku akitenda kama nabii mpaka alipoingia Naiothi kule Rama. 24 Akararua pia mavazi yake, naye pia akatenda kama nabii mbele ya Samweli, akalala huko mchana wote na usiku huo wote akiwa uchi.* Ndiyo sababu wanasema: “Je, Sauli pia ni mmoja wa manabii?”+

20 Kisha Daudi akakimbia kutoka Naiothi huko Rama. Hata hivyo, akaenda kwa Yonathani na kumuuliza: “Nimefanya nini?+ Nimefanya kosa gani, nami nimemtendea baba yako dhambi gani hivi kwamba anataka kuniua?” 2 Yonathani akamwambia: “Ni jambo lisiloweza kuwaziwa kamwe!+ Hutakufa. Baba yangu hawezi kufanya jambo lolote, liwe kubwa au dogo, bila kuniambia. Kwa nini baba yangu anifiche jambo hilo? Hawezi kufanya hivyo.” 3 Lakini Daudi akaapa hivi tena: “Bila shaka baba yako anajua kwamba unanipenda+ na hivyo atasema, ‘Msimwambie Yonathani jambo hili asije akahuzunika.’ Lakini kwa hakika kama Yehova anavyoishi na kwa hakika kama unavyoishi,* kuna hatua moja tu kati yangu na kifo!”+

4 Ndipo Yonathani akamwambia Daudi: “Nitakufanyia lolote unalosema.” 5 Daudi akamwambia Yonathani: “Kesho ni mwezi mpya,+ na hakika ninatazamiwa kuketi pamoja na mfalme ili kula naye; niache niende, nitajificha shambani mpaka siku ya tatu jioni. 6 Ikiwa baba yako atanikosa, mwambie, ‘Daudi alinisihi nimruhusu aende mara moja katika jiji lake la Bethlehemu,+ kwa sababu kuna dhabihu ya kila mwaka huko kwa ajili ya familia yote.’+ 7 Akisema, ‘Ni vema!’ mimi mtumishi wako nitakuwa na amani. Lakini akikasirika, uwe na hakika kwamba ameazimia kunidhuru. 8 Nitendee mimi mtumishi wako kwa upendo mshikamanifu,+ kwa kuwa umeniingiza mimi mtumishi wako katika agano ulilofanya na Yehova.+ Lakini ikiwa nina hatia,+ niue wewe mwenyewe. Kwa nini unitie mikononi mwa baba yako?”

9 Kwa hiyo Yonathani akasema: “Ni jambo nisiloweza kamwe kuwazia kwamba nipendekeze utendewe hivyo! Nikipata habari kwamba baba yangu ameazimia kukudhuru, kwa nini nisikwambie?”+ 10 Kisha Daudi akamuuliza Yonathani: “Ni nani atakayeniambia baba yako akikujibu kwa ukali?” 11 Yonathani akamwambia Daudi: “Njoo, twende shambani.” Basi wote wawili wakaenda shambani. 12 Yonathani akamwambia Daudi: “Yehova Mungu wa Israeli na awe shahidi kwamba nitamchunguza baba yangu wakati kama huu kesho au siku ya tatu. Ikiwa ana mtazamo mzuri kukuelekea, je, sitakujulisha au kukufunulia jambo hilo? 13 Lakini ikiwa baba yangu anakusudia kukudhuru, Yehova na aniadhibu, tena vikali, ikiwa sitakufunulia jambo hilo na kuacha uende zako kwa amani. Yehova na awe pamoja nawe,+ kama alivyokuwa na baba yangu.+ 14 Na je, hutanitendea kwa upendo mshikamanifu wa Yehova ningali hai na hata nikifa?+ 15 Usiache kamwe kuitendea nyumba yangu kwa upendo mshikamanifu,+ hata Yehova atakapowafagilia mbali maadui wote wa Daudi duniani pote.” 16 Basi Yonathani akafanya agano pamoja na nyumba ya Daudi, akisema: “Yehova atadai jambo hilo na kuwaadhibu maadui wa Daudi.” 17 Basi Yonathani akamwapisha tena Daudi kwa msingi wa upendo aliokuwa nao kumwelekea, kwa sababu alimpenda kama alivyojipenda mwenyewe.*+

18 Kisha Yonathani akamwambia: “Kesho ni mwezi mpya,+ nawe utakosekana kwa sababu kiti chako kitakuwa wazi. 19 Kufikia siku ya tatu, wataona wazi kwamba haupo, utakuja mahali hapa ulipojificha ile siku nyingine* na ukae hapa karibu na jiwe. 20 Kisha nitapiga mishale mitatu upande mmoja wa jiwe hili kana kwamba ninalenga shabaha fulani. 21 Nitakapomtuma mtumishi, nitasema, ‘Nenda, ukaitafute mishale.’ Nikimwambia mtumishi, ‘Angalia! Mishale iko upande huu wako, ichukue,’ basi unaweza kurudi, kwa maana kwa hakika kama Yehova anavyoishi, hilo linamaanisha kwamba kuna amani katika mambo yako yote na hakuna hatari. 22 Lakini nikimwambia mvulana huyo, ‘Angalia! Mishale iko mbele yako,’ basi ondoka, kwa sababu Yehova anataka uende zako. 23 Kuhusu ahadi ambayo tumeweka,+ mimi na wewe, Yehova na awe kati yetu milele.”+

24 Basi Daudi akajificha shambani. Mwezi mpya ulipofika, mfalme aliketi kwenye kiti chake ili ale.+ 25 Mfalme alikuwa ameketi mahali pake alipoketi kwa kawaida karibu na ukuta. Yonathani aliketi kumwelekea, na Abneri+ aliketi kando ya Sauli, lakini mahali pa Daudi palikuwa wazi. 26 Sauli hakusema lolote siku hiyo, kwa maana alisema moyoni mwake: ‘Jambo fulani limetokea ambalo limemfanya asiwe safi.+ Naam, yeye si safi.’ 27 Siku ya pili baada ya mwezi mpya, bado mahali pa Daudi palikuwa wazi. Kwa hiyo Sauli akamuuliza Yonathani mwana wake: “Kwa nini mwana wa Yese+ hakuja kwenye mlo jana wala leo?” 28 Yonathani akamjibu Sauli: “Daudi alinisihi nimruhusu aende Bethlehemu.+ 29 Aliniambia, ‘Tafadhali niruhusu niende, kwa sababu tuna dhabihu ya familia jijini, na ndugu yangu mwenyewe aliniita. Basi ikiwa nimepata kibali machoni pako, tafadhali acha niende kisiri nikawaone ndugu zangu.’ Ndiyo sababu hajaja kwenye meza ya mfalme.” 30 Kisha Sauli akamkasirikia Yonathani na kumwambia: “Wewe mwana wa mwanamke mwasi, unafikiri sijui kwamba umeamua kumuunga mkono mwana wa Yese, kwa aibu yako mwenyewe na kwa aibu ya mama yako?* 31 Maadamu mwana wa Yese anaishi duniani, wewe wala ufalme wako hautadumu.+ Basi sasa mtume mtu fulani amlete kwangu, kwa maana lazima afe.”*+

32 Hata hivyo, Yonathani akamwambia Sauli baba yake: “Kwa nini auawe?+ Amefanya nini?” 33 Ndipo Sauli akamtupia mkuki ili amuue,+ basi Yonathani akajua kwamba baba yake alikuwa ameazimia kumuua Daudi.+ 34 Yonathani akainuka mara moja kutoka mezani akiwa amekasirika sana, naye hakula chakula chochote siku ya pili baada ya mwezi mpya, kwa maana alikuwa amehuzunika sana kwa sababu ya Daudi+ na kwa sababu baba yake mwenyewe alikuwa amemwaibisha.

35 Asubuhi Yonathani akaenda shambani kukutana na Daudi kama walivyokubaliana, na mtumishi fulani kijana alikuwa pamoja naye.+ 36 Akamwambia mtumishi wake: “Tafadhali kimbia utafute mishale nitakayopiga.” Mtumishi huyo akakimbia, kisha Yonathani akapiga mshale mbele yake. 37 Mtumishi huyo alipofika mahali ambapo Yonathani alikuwa amepiga mshale, Yonathani akamwambia hivi mtumishi huyo kwa sauti: “Mshale uko mbele yako!” 38 Yonathani akaendelea kumwambia mtumishi huyo kwa sauti: “Fanya haraka! Kimbia! Usikawie!” Mtumishi wa Yonathani akaiokota ile mishale na kurudi kwa bwana wake. 39 Lakini mtumishi huyo hakuelewa lolote kuhusu jambo hilo; Yonathani na Daudi peke yao ndio walioelewa jambo hilo. 40 Kisha Yonathani akampa mtumishi wake silaha zake na kumwambia: “Nenda, zipeleke jijini.”

41 Mtumishi huyo alipoondoka, Daudi akatoka mahali alipokuwa amejificha hapo karibu upande wa kusini. Kisha akaanguka chini kifudifudi na kuinama mara tatu, nao wakabusiana na kulia pamoja, lakini Daudi alilia zaidi. 42 Yonathani akamwambia Daudi: “Nenda kwa amani, kwa maana sote wawili tumeapa+ kwa jina la Yehova tukisema, ‘Yehova na awe kati yangu na wewe na kati ya uzao wangu* na uzao wako* milele.’”+

Kisha Daudi akainuka na kuondoka, naye Yonathani akarudi jijini.

21 Baadaye Daudi akafika Nobu+ kwa kuhani Ahimeleki. Ahimeleki alianza kutetemeka alipokutana na Daudi, akamuuliza: “Kwa nini uko peke yako na hujaja na mtu yeyote?”+ 2 Daudi akamjibu kuhani Ahimeleki: “Mfalme aliniagiza nifanye jambo fulani, lakini akaniambia, ‘Usimjulishe mtu yeyote kazi niliyokutuma kufanya na maagizo niliyokupa.’ Nilikubaliana na vijana wangu tukutane mahali fulani. 3 Sasa ikiwa una mikate mitano, nipe tu, au chochote kinachopatikana.” 4 Lakini kuhani akamwambia Daudi: “Kwa sasa hakuna mikate ya kawaida, lakini kuna mikate mitakatifu+—ninaweza kukupa tu ikiwa vijana wako wamejiepusha na wanawake.”*+ 5 Daudi akamwambia hivi kuhani: “Kwa hakika tumejitenga kabisa na wanawake kama tulivyofanya awali nilipoenda vitani.+ Ikiwa miili ya vijana hawa ni mitakatifu hata katika shughuli za kawaida, je, si mitakatifu zaidi leo?” 6 Basi kuhani akampa mikate mitakatifu,+ kwa sababu hakukuwa na mikate mingine isipokuwa mikate ya wonyesho iliyokuwa imeondolewa mbele za Yehova na mikate mipya kuwekwa siku hiyo.

7 Basi mmoja wa watumishi wa Sauli alikuwa hapo siku hiyo, akiwa amezuiliwa mbele za Yehova. Aliitwa Doegi+ Mwedomu,+ mkuu wa wachungaji wa Sauli.

8 Basi Daudi akamuuliza Ahimeleki: “Je, una mkuki au upanga hapa? Sikubeba upanga wangu wala silaha zangu kwa sababu kazi ya mfalme ilipaswa kufanywa haraka.” 9 Ndipo kuhani akamwambia: “Nina upanga wa Goliathi+ yule Mfilisti, uliyemuua katika Bonde la* Ela,+ nao umefungwa kwa kitambaa nyuma ya efodi.+ Ikiwa unataka kuuchukua, uchukue, kwa sababu ndio upanga pekee ulio hapa.” Daudi akamwambia: “Hakuna upanga mwingine kama huo. Nipe upanga huo.”

10 Siku hiyo Daudi akaondoka na kuendelea kumkimbia+ Sauli, hatimaye akafika kwa Mfalme Akishi wa Gathi.+ 11 Watumishi wa Akishi wakamuuliza Akishi: “Je, huyu si Daudi mfalme wa ile nchi? Je, si yeye waliyeimba kumhusu walipocheza dansi, wakisema,

‘Sauli ameua maelfu yake,

Na Daudi makumi yake ya maelfu’?”+

12 Daudi akayaweka maneno hayo moyoni mwake, naye akamwogopa sana+ Mfalme Akishi wa Gathi. 13 Kwa hiyo akajifanya hana akili timamu+ mbele yao na kutenda kama mwenda wazimu kati yao.* Alikuwa akitia alama kwenye milango ya lango na kuacha mate yake yatiririke kwenye ndevu zake. 14 Mwishowe Akishi akawaambia watumishi wake: “Hamwoni kwamba mtu huyu ni mwenda wazimu? Kwa nini mmemleta kwangu? 15 Je, nimepungukiwa na wenda wazimu hivi kwamba nahitaji mtu huyu atende kiwazimu mbele yangu? Kwa nini ameingia nyumbani mwangu?”

22 Basi Daudi akaondoka huko+ na kukimbilia katika pango la Adulamu.+ Ndugu zake na nyumba yote ya baba yake waliposikia habari hiyo, wakashuka na kumfuata huko. 2 Na watu wote waliokuwa na shida na madeni na malalamishi* wakakusanyika kwake, akawa kiongozi wao. Watu 400 hivi walikuwa pamoja naye.

3 Baadaye Daudi akaondoka huko na kwenda Mispe kule Moabu na kumwambia hivi mfalme wa Moabu:+ “Tafadhali mruhusu baba yangu na mama yangu wakae pamoja nawe mpaka nitakapojua Mungu atanifanyia nini.” 4 Basi akawaacha wakae na mfalme wa Moabu, nao wakakaa naye muda wote ambao Daudi alikuwa ndani ya ngome.+

5 Baada ya muda nabii Gadi+ akamwambia Daudi: “Usikae ndani ya ngome. Ondoka humo uende katika nchi ya Yuda.”+ Kwa hiyo Daudi akaondoka na kwenda katika msitu wa Herethi.

6 Sauli akasikia kwamba Daudi na watu waliokuwa pamoja naye wameonekana. Wakati huo Sauli alikuwa ameketi kwenye kilima chini ya mti wa mwesheli kule Gibea+ akiwa ameshika mkuki wake mkononi, na watumishi wake wote walikuwa wamemzunguka. 7 Ndipo Sauli akawaambia watumishi wake waliokuwa wamemzunguka: “Tafadhali sikilizeni, enyi Wabenjamini. Je, mwana wa Yese+ atawapa ninyi nyote pia mashamba na mashamba ya mizabibu? Je, atawaweka nyote kuwa wakuu wa maelfu na wakuu wa mamia?+ 8 Ninyi nyote mmepanga njama dhidi yangu! Hakuna yeyote aliyenijulisha wakati mwana wangu mwenyewe alipofanya agano na mwana wa Yese!+ Hakuna yeyote kati yenu anayenihurumia na kunijulisha kwamba mwanangu mwenyewe amemchochea mtumishi wangu mwenyewe dhidi yangu ili anivizie, kama hali ilivyo sasa.”

9 Kisha Doegi+ Mwedomu, aliyekuwa hapo akiwa msimamizi wa watumishi wa Sauli, akamjibu hivi:+ “Nilimwona mwana wa Yese akija Nobu kwa Ahimeleki mwana wa Ahitubu.+ 10 Naye akamwombea Daudi mwongozo kutoka kwa Yehova na kumpa vyakula. Hata alimpa upanga wa Goliathi yule Mfilisti.”+ 11 Mara moja mfalme akaagiza Ahimeleki mwana wa kuhani Ahitubu na makuhani wote wa nyumba ya baba yake waliokuwa Nobu waitwe. Basi wote wakaja kwa mfalme.

12 Sasa Sauli akasema: “Sikiliza, tafadhali, wewe mwana wa Ahitubu!” naye akajibu: “Naam, bwana wangu.” 13 Sauli akamwambia: “Kwa nini mmepanga njama dhidi yangu, wewe na mwana wa Yese, kwa kumpa mikate na upanga na kumtafutia mwongozo kutoka kwa Mungu? Yeye hunipinga na kunivizia, kama anavyofanya sasa.” 14 Ndipo Ahimeleki akamjibu hivi mfalme: “Ni nani kati ya watumishi wako wote anayeaminika* kama Daudi?+ Yeye ni mkwe wako+ mfalme na mkuu wa walinzi wako na anaheshimika katika nyumba yako.+ 15 Je, unafikiri kwamba leo ndio mara ya kwanza kwangu kumtafutia mwongozo kutoka kwa Mungu?+ Jambo unalosema, ni jambo nisiloweza kamwe kuwazia! Nakusihi mfalme usinikasirikie mimi mtumishi wako na nyumba yote ya baba yangu, kwa maana mimi mtumishi wako sikujua lolote kati ya mambo haya.”+

16 Lakini mfalme akasema: “Hakika utakufa+ Ahimeleki, wewe pamoja na nyumba yote ya baba yako.”+ 17 Ndipo mfalme akawaambia walinzi* waliomzunguka: “Geukeni na kuwaua makuhani wa Yehova, kwa sababu wamemuunga mkono Daudi! Walijua kwamba ametoroka, lakini hawakunijulisha!” Lakini watumishi hao wa mfalme hawakutaka kuinua mikono yao wawashambulie makuhani wa Yehova. 18 Basi mfalme akamwambia Doegi:+ “Wewe geuka uwashambulie makuhani!” Mara moja Doegi Mwedomu+ akageuka na kuwashambulia hao makuhani yeye mwenyewe. Siku hiyo aliwaua wanaume 85 waliovaa efodi ya kitani.+ 19 Pia, akalishambulia kwa upanga jiji la Nobu,+ jiji la makuhani; aliwaua kwa upanga wanaume na wanawake, watoto wadogo na wale wanaonyonya, ng’ombe dume, punda, na kondoo.

20 Hata hivyo, mwana mmoja wa Ahimeleki mwana wa Ahitubu, aliyeitwa Abiathari,+ akatoroka, akakimbia kumfuata Daudi. 21 Abiathari akamwambia hivi Daudi: “Sauli amewaua makuhani wa Yehova.” 22 Ndipo Daudi akamwambia Abiathari: “Siku ile,+ Doegi Mwedomu alipokuwa huko, nilijua kwa hakika kwamba atamwambia Sauli. Mimi binafsi ninawajibika kwa sababu ya kifo cha kila mtu* katika nyumba ya baba yako. 23 Kaa pamoja nami. Usiogope, kwa kuwa yeyote anayetafuta uhai wako* anatafuta uhai wangu;* nitakulinda.”+

23 Baada ya muda Daudi aliambiwa hivi: “Wafilisti wanashambulia Keila,+ nao wanapora nafaka kwenye viwanja vya kupuria.” 2 Basi Daudi akamuuliza Yehova:+ “Je, niende nikawaue Wafilisti hawa?” Yehova akamwambia Daudi: “Nenda, waue Wafilisti hao na kuokoa Keila.” 3 Lakini wanaume wa Daudi wakamwambia: “Tazama! Ikiwa tunaogopa tukiwa hapa Yuda,+ itakuwaje tukienda Keila kupigana na vikosi vya Wafilisti?”+ 4 Kwa hiyo Daudi akamwomba tena Yehova ushauri.+ Sasa Yehova akamjibu hivi: “Ondoka, ushuke kwenda Keila kwa sababu nitawatia Wafilisti mikononi mwako.”+ 5 Basi Daudi akaenda na wanaume wake Keila na kupigana na Wafilisti; akachukua mifugo yao na kuwaua Wafilisti wengi sana, Daudi akawaokoa wakaaji wa Keila.+

6 Sasa Abiathari+ mwana wa Ahimeleki alipokimbia kwenda kwa Daudi huko Keila, alikuwa na efodi. 7 Sauli akaambiwa hivi: “Daudi amekuja Keila.” Sauli akasema: “Mungu amemtia mikononi mwangu,*+ kwa maana amejiingiza mwenyewe ndani ya mtego kwa kuingia katika jiji lenye milango na makomeo.” 8 Kwa hiyo Sauli akawakusanya watu wote waende vitani, washuke Keila na kumzingira Daudi na wanaume wake. 9 Daudi alipopata habari kwamba Sauli alikuwa akipanga njama dhidi yake, akamwambia kuhani Abiathari: “Ilete efodi hapa.”+ 10 Kisha Daudi akasema: “Ee Yehova Mungu wa Israeli, mimi mtumishi wako nimesikia kwa hakika kwamba Sauli anakusudia kuja Keila kuliangamiza jiji hili kwa sababu yangu.+ 11 Je, viongozi* wa Keila watanitia mikononi mwake? Je, Sauli atashuka kuja hapa kama mimi mtumishi wako nilivyosikia? Ee Yehova Mungu wa Israeli, tafadhali nijulishe mimi mtumishi wako.” Ndipo Yehova akamwambia: “Atashuka.” 12 Daudi akauliza: “Je, viongozi wa Keila watanitia mimi na wanaume wangu mikononi mwa Sauli?” Yehova akajibu: “Watakutia mikononi mwake.”

13 Mara moja Daudi akainuka pamoja na wanaume wake, wapatao 600,+ wakaondoka Keila na kwenda popote walipoweza kwenda. Sauli alipoambiwa kwamba Daudi ametoroka Keila, hakumfuatia. 14 Daudi akakaa nyikani katika sehemu ambazo hazifikiki kwa urahisi, kwenye eneo lenye milima katika nyika ya Zifu.+ Sauli aliendelea kumtafuta,+ lakini Yehova hakumtia Daudi mikononi mwake. 15 Daudi alijua kwamba* Sauli alikuwa akimtafuta ili amuue* Daudi alipokuwa katika nyika ya Zifu huko Horeshi.

16 Sasa Yonathani mwana wa Sauli akaenda kumwona Daudi huko Horeshi, akamsaidia kupata nguvu* katika Yehova.+ 17 Akamwambia: “Usiogope, kwa maana Sauli baba yangu hatakupata; utakuwa mfalme wa Israeli,+ nami nitakuwa wa pili baada yako; na Sauli baba yangu anajua jambo hilo.”+ 18 Kisha wote wawili wakafanya agano+ mbele za Yehova, na Daudi akaendelea kukaa Horeshi, naye Yonathani akaenda nyumbani kwake.

19 Baadaye watu wa Zifu wakapanda kwenda kwa Sauli kule Gibea+ na kumwambia: “Daudi anajificha karibu nasi+ katika sehemu ambazo hazifikiki kwa urahisi kule Horeshi,+ kwenye kilima cha Hakila,+ kilicho upande wa kusini* wa Yeshimoni.*+ 20 Wakati wowote utakaopenda kushuka huko, Ee mfalme, shuka, nasi tutamtia mikononi mwako mfalme.”+ 21 Ndipo Sauli akasema: “Yehova na awabariki kwa sababu mmenihurumia. 22 Tafadhali nendeni mjaribu kutafuta mahali hususa alipo na mtu aliyemwona huko, kwa sababu nimeambiwa kwamba yeye ni mjanja sana. 23 Chunguzeni kwa makini kila mahali anapojificha na mrudi kwangu mkiwa na ushahidi. Kisha nitaenda pamoja nanyi, na ikiwa yuko nchini, nitamsaka kabisa miongoni mwa maelfu yote ya* Yuda.”

24 Basi wakaondoka na kumtangulia Sauli kwenda Zifu,+ na wakati huo Daudi na wanaume wake walikuwa katika nyika ya Maoni,+ kule Araba+ upande wa kusini wa Yeshimoni. 25 Kisha Sauli akaja na wanaume wake kumtafuta.+ Daudi alipoambiwa jambo hilo, akashuka mara moja na kwenda kwenye mwamba,+ naye akakaa katika nyika ya Maoni. Sauli aliposikia hilo, akamfuatia Daudi katika nyika ya Maoni. 26 Sauli alipofika upande mmoja wa mlima, Daudi na wanaume wake walikuwa upande wa pili wa mlima huo. Daudi alikuwa akifanya haraka kumkimbia+ Sauli, lakini Sauli na wanaume wake walikuwa wakimkaribia Daudi na wanaume wake ili wawakamate.+ 27 Lakini mjumbe fulani akaja kwa Sauli na kumwambia: “Njoo haraka, kwa sababu Wafilisti wameivamia nchi!” 28 Ndipo Sauli akaacha kumfuatia Daudi,+ akaenda kukabiliana na Wafilisti. Ndiyo sababu mahali hapo paliitwa Mwamba wa Migawanyiko.

29 Kisha Daudi akapanda kutoka huko na kwenda kukaa katika sehemu ambazo hazifikiki kwa urahisi kule En-gedi.+

24 Mara tu Sauli aliporudi baada ya kuwafuatia Wafilisti, aliambiwa hivi: “Tazama! Daudi yuko katika nyika ya En-gedi.”+

2 Basi Sauli akachukua wanaume 3,000 mashujaa kutoka nchi yote ya Israeli na kwenda kumtafuta Daudi na wanaume wake kwenye miamba ya mbuzi wa milimani. 3 Sauli akafika kwenye mazizi ya kondoo yaliyojengwa kwa mawe kando ya barabara, mahali ambapo palikuwa na pango, akaingia pangoni kwenda haja,* wakati huo Daudi na wanaume wake walikuwa wameketi ndani kabisa ya pango hilo.+ 4 Wanaume wa Daudi wakamwambia: “Hii ndiyo siku ambayo Yehova anakwambia, ‘Tazama! Ninamtia adui yako mikononi mwako,+ nawe unaweza kumtendea jambo lolote unalotaka.’” Kwa hiyo Daudi akasimama, akakata kimyakimya upindo wa joho la Sauli lisilo na mikono. 5 Lakini baadaye moyo wa Daudi ukaendelea kumchoma*+ kwa sababu alikuwa amekata upindo wa joho la Sauli lisilo na mikono. 6 Akawaambia wanaume wake: “Siwezi kamwe kuwazia, kulingana na maoni ya Yehova, kumtendea jambo kama hilo bwana wangu, mtiwa-mafuta wa Yehova, kwa kuinua mkono wangu dhidi yake, kwa kuwa yeye ni mtiwa-mafuta wa Yehova.”+ 7 Basi Daudi akawazuia* wanaume wake kwa maneno hayo, naye hakuwaruhusu wamshambulie Sauli. Sauli akaondoka pangoni na kwenda zake.

8 Baadaye Daudi akainuka na kutoka pangoni, akamwita Sauli: “Bwana wangu mfalme!”+ Sauli alipoangalia nyuma, Daudi aliinama hadi chini kifudifudi na kusujudu. 9 Daudi akamuuliza Sauli: “Kwa nini unasikiliza maneno ya watu wanaosema, ‘Tazama! Daudi anataka kukudhuru’?+ 10 Siku hii ya leo umeona kwa macho yako mwenyewe jinsi Yehova alivyokutia mikononi mwangu pangoni. Lakini mtu fulani aliposema nikuue,+ nilikusikitikia nikasema, ‘Sitainua mkono wangu dhidi ya bwana wangu, kwa maana yeye ni mtiwa-mafuta wa Yehova.’+ 11 Tazama baba yangu, angalia nimeshika upindo wa joho lako lisilo na mikono; kwa sababu nilipokata upindo wa joho lako lisilo na mikono, sikukuua. Sasa unaweza kuona na kuelewa kwamba sikusudii kukudhuru wala kukuasi, nami sijakutendea dhambi,+ lakini wewe unaniwinda ili kuniua.*+ 12 Yehova na ahukumu kati yangu na wewe,+ na Yehova anilipizie kisasi mambo unayonitendea,+ lakini sitainua mkono wangu dhidi yako.+ 13 Kama methali ya kale inavyosema, ‘Kutoka kwa mwovu hutoka uovu,’ lakini sitainua mkono wangu dhidi yako. 14 Mfalme wa Israeli ametoka kumtafuta nani? Unamfuatia nani? Mbwa aliyekufa? Kiroboto mmoja?+ 15 Yehova na awe mwamuzi, atahukumu kati yangu na wewe, naye ataona na kunitetea na kuamua kesi yangu+ na kuniokoa kutoka mikononi mwako.”

16 Mara tu Daudi alipomaliza kumwambia maneno hayo, Sauli akasema: “Je, hiyo ni sauti yako, Daudi mwanangu?”+ Kisha Sauli akaanza kulia kwa sauti kubwa. 17 Akamwambia Daudi: “Wewe ni mwadilifu kuliko mimi, kwa maana umenitendea mema lakini mimi nimekulipa kwa uovu.+ 18 Naam, leo umeniambia mema uliyotenda kwa kukosa kuniua Yehova aliponitia mikononi mwako.+ 19 Ni mtu gani anayempata adui yake na kumwacha aende zake bila kumdhuru? Yehova atakuthawabisha wewe kwa mema+ kwa sababu ya mambo uliyonifanyia leo. 20 Sasa tazama! Najua kwa hakika kwamba utatawala ukiwa mfalme+ na kwamba ufalme wa Israeli utadumu mikononi mwako. 21 Sasa niapie mbele za Yehova+ kwamba hutawafagilia mbali wazao wangu* baada yangu na kwamba hutalifutilia mbali jina langu kutoka katika nyumba ya baba yangu.”+ 22 Kwa hiyo Daudi akamwapia Sauli, kisha Sauli akaenda nyumbani kwake.+ Lakini Daudi na wanaume wake wakapanda kwenda ndani ya ngome.+

25 Baada ya muda Samweli+ akafa; na Waisraeli wote wakakusanyika pamoja kumwombolezea na kumzika nyumbani kwake huko Rama.+ Kisha Daudi akaondoka na kushuka kwenda katika nyika ya Parani.

2 Sasa kulikuwa na mtu fulani kule Maoni+ aliyekuwa akifanya kazi Karmeli.*+ Mtu huyo alikuwa tajiri sana; alikuwa na kondoo 3,000 na mbuzi 1,000, naye alikuwa akiwakata kondoo wake manyoya huko Karmeli. 3 Mtu huyo aliitwa Nabali,+ na mke wake aliitwa Abigaili.+ Mke huyo alikuwa mwenye busara* na mrembo, lakini mume wake, Mkalebu,+ alikuwa mkali na mwenye tabia mbaya.+ 4 Daudi akasikia akiwa nyikani kwamba Nabali alikuwa akiwakata kondoo wake manyoya. 5 Kwa hiyo Daudi akawatuma vijana kumi wanaume waende kwa Nabali, akawaambia: “Pandeni mwende Karmeli, na mtakapofika kwa Nabali, mjulieni hali yake kwa jina langu. 6 Kisha mwambieni, ‘Uishi maisha marefu na uwe na amani na nyumba yako iwe na amani na vitu vyako vyote viwe na amani. 7 Sasa nimesikia kwamba unawakata kondoo wako manyoya. Wachungaji wako walipokuwa pamoja nasi hatukuwadhuru,+ na wakati wote walipokuwa Karmeli hawakupoteza chochote. 8 Waulize vijana wako, nao watakwambia. Vijana wangu na wapate kibali machoni pako, kwa sababu tumekuja wakati wa shangwe.* Tafadhali tupatie sisi watumishi wako na Daudi mwana wako chochote unachoweza kumpa.’”+

9 Basi vijana wa Daudi wakaenda na kumwambia Nabali mambo yote hayo kwa jina la Daudi. Walipomaliza, 10 Nabali akawajibu hivi watumishi wa Daudi: “Daudi ni nani, na mwana wa Yese ni nani? Siku hizi watumishi wengi wanawatoroka mabwana zao.+ 11 Ninawezaje kuchukua mikate yangu na maji yangu na nyama niliyowachinjia wakataji manyoya wangu na kuwapa watu ambao hata hawajulikani wanatoka wapi?”

12 Kwa hiyo vijana wa Daudi wakarudi na kumwambia Daudi maneno hayo yote. 13 Mara moja Daudi akawaambia wanaume wake: “Kila mtu ajifunge upanga wake!”+ Basi wote wakajifunga panga zao, na Daudi pia akajifunga upanga wake mwenyewe, na wanaume wapatao 400 wakapanda pamoja na Daudi, huku wanaume 200 wakibaki na mizigo.

14 Wakati huo, mtumishi mmoja akamletea Abigaili mke wa Nabali habari hii: “Tazama! Daudi aliwatuma wajumbe kutoka nyikani ili kumtakia mema bwana wetu, lakini aliwatukana vikali.+ 15 Wanaume hao walitutendea kwa wema sana. Hawakutudhuru kamwe, nasi hatukukosa hata kitu kimoja wakati wote tulipokuwa nao malishoni.+ 16 Walikuwa kama ukuta wa ulinzi kutuzunguka, usiku na mchana, wakati wote tulipokuwa nao tukichunga kondoo. 17 Sasa amua utakalofanya, kwa maana kwa hakika bwana wetu ataangamizwa pamoja na nyumba yake yote,+ naye ni mtu asiyefaa kitu* hivi+ kwamba hakuna mtu anayeweza kuzungumza naye.”

18 Basi Abigaili+ akachukua haraka mikate 200, mitungi miwili mikubwa ya divai, kondoo watano waliochinjwa, sea tano* za nafaka iliyokaangwa, keki 100 za zabibu kavu, na keki 200 za tini zilizoshinikizwa, akapakia vitu hivyo vyote juu ya punda.+ 19 Kisha akawaambia watumishi wake: “Tangulieni; nitawafuata.” Lakini hakumwambia Nabali mumewe jambo lolote.

20 Abigaili alipokuwa juu ya punda akishuka bondeni nyuma ya mlima, alikutana kwa ghafla na Daudi na wanaume wake wakishuka kumwelekea. 21 Sasa Daudi alikuwa akisema: “Ilikuwa kazi ya bure kulinda mali yote ya mtu huyu nyikani. Hakuna kitu chake hata kimoja kilichopotea,+ lakini ananilipa uovu kwa wema niliomfanyia.+ 22 Mungu na awaadhibu, tena vikali, maadui wa Daudi* ikiwa nitamwacha mwanamume wake yeyote* abaki hai mpaka asubuhi.”

23 Abigaili alipomwona Daudi, alishuka haraka kutoka juu ya punda na kuanguka kifudifudi mbele ya Daudi, huku akiinama chini. 24 Kisha akaanguka miguuni pake na kusema: “Bwana wangu, acha nibebe lawama; niruhusu mimi kijakazi wako nizungumze nawe, na usikilize maneno ya kijakazi wako. 25 Tafadhali, bwana wangu usimsikilize huyu Nabali asiyefaa kitu,+ kwa maana jina lake linamfaa kabisa. Anaitwa Nabali,* na kwa kweli ni mtu mpumbavu. Lakini mimi kijakazi wako, sikuwaona vijana wako bwana wangu, uliowatuma. 26 Na sasa, bwana wangu, kwa hakika kama Yehova anavyoishi na kama wewe unavyoishi, Yehova ndiye amekuzuia+ usiwe na hatia ya damu+ na usilipize kisasi* kwa mkono wako mwenyewe. Maadui wako na wale wanaotaka kukudhuru bwana wangu na wawe kama Nabali. 27 Sasa pokea zawadi*+ hii ambayo mimi kijakazi wako nimekuletea bwana wangu na uwape vijana wanaokufuata bwana wangu.+ 28 Tafadhali, nisamehe kosa langu mimi kijakazi wako, kwa maana hakika Yehova atakujengea wewe bwana wangu nyumba inayodumu,+ kwa sababu wewe bwana wangu unapigana vita vya Yehova,+ na uovu haujaonekana ndani yako siku zako zote.+ 29 Mtu akiinuka ili akufuatie na kuutafuta uhai wako,* Yehova Mungu wako atakuwa ameufungia salama uhai wako* katika mfuko wa uzima, bwana wangu, lakini atautupa mbali uhai wa maadui wako kama mawe yanavyotupwa kwa kombeo. 30 Na baada ya Yehova kukufanyia wewe bwana wangu mambo yote mema aliyoahidi na kukuweka kuwa kiongozi wa Israeli,+ 31 hutahuzunika wala kujuta moyoni mwako kwa sababu ya kumwaga damu bila sababu na kulipiza kisasi*+ kwa mkono wako bwana wangu. Yehova atakapokutendea mema bwana wangu, nikumbuke mimi kijakazi wako.”

32 Ndipo Daudi akamwambia Abigaili: “Msifu Yehova Mungu wa Israeli, aliyekutuma leo ukutane nami! 33 Busara yako na ibarikiwe! Na ubarikiwe kwa kunizuia leo nisiwe na hatia ya damu+ na nisilipize kisasi* kwa mikono yangu mwenyewe. 34 La sivyo, kwa hakika kama Yehova Mungu wa Israeli anavyoishi aliyenizuia nisikudhuru,+ ikiwa hungekuja haraka kukutana nami,+ kufikia asubuhi hakuna mwanamume hata mmoja* wa Nabali angekuwa hai.”+ 35 Basi Daudi akapokea vitu ambavyo Abigaili alikuwa amemletea na kumwambia: “Panda uende nyumbani kwako kwa amani. Tazama, nimekusikiliza na nitatimiza ombi lako.”

36 Baadaye Abigaili akarudi kwa Nabali, naye Nabali alikuwa akila na kunywa kama mfalme nyumbani mwake, na alikuwa amechangamka sana* na kulewa kabisa. Lakini Abigaili hakumwambia jambo lolote mpaka asubuhi kulipopambazuka. 37 Asubuhi, divai ilipokuwa imemtoka Nabali, mke wake akamwambia mambo hayo. Na moyo wa Nabali ukawa kama wa mtu aliyekufa, akalala akiwa amepooza kama jiwe. 38 Siku kumi hivi baadaye, Yehova akampiga Nabali, naye akafa.

39 Daudi aliposikia kwamba Nabali amekufa, akasema: “Asifiwe Yehova, ambaye amenitetea+ baada ya kuaibishwa na Nabali,+ na amenizuia mimi mtumishi wake nisitende jambo lolote ovu,+ na Yehova amemwadhibu Nabali kwa sababu ya uovu wake!”* Kisha Daudi akawatuma wajumbe kwa Abigaili akiomba awe mke wake. 40 Basi watumishi wa Daudi wakafika kwa Abigaili huko Karmeli na kumwambia: “Daudi ametutuma kwako ili tukuchukue uwe mke wake.” 41 Mara moja akasimama na kuinama chini kifudifudi na kusema: “Nipo hapa mimi mtumwa wako, ili niwe kijakazi wa kuwaosha miguu+ watumishi wa bwana wangu.” 42 Kisha Abigaili+ akasimama haraka na kupanda juu ya punda wake na vijakazi wake watano walitembea nyuma yake; alienda pamoja na wajumbe wa Daudi, akawa mke wake.

43 Daudi alikuwa pia amemwoa Ahinoamu+ kutoka Yezreeli,+ na wanawake wote wawili wakawa wake zake.+

44 Lakini Sauli alikuwa amemchukua Mikali binti yake,+ mke wa Daudi na kumpa Palti+ mwana wa Laishi, kutoka Galimu.

26 Baada ya muda watu wa Zifu+ wakaja kwa Sauli huko Gibea,+ wakisema: “Daudi amejificha kwenye kilima cha Hakila, ng’ambo ya Yeshimoni.”*+ 2 Basi Sauli akaondoka na kushuka kwenda katika nyika ya Zifu akiwa na wanaume 3,000 mashujaa wa Israeli ili kumtafuta Daudi katika nyika ya Zifu.+ 3 Sauli akapiga kambi kwenye kilima cha Hakila, kilicho ng’ambo ya Yeshimoni, kando ya barabara. Wakati huo Daudi alikuwa akiishi nyikani, akapata habari kwamba Sauli alikuwa amekuja nyikani kumtafuta. 4 Basi Daudi akatuma wapelelezi ili wathibitishe kwamba kwa kweli Sauli alikuwa amekuja. 5 Baadaye Daudi akaenda mahali ambapo Sauli alikuwa amepiga kambi, na Daudi akaona mahali ambapo Sauli na Abneri+ mwana wa Neri, mkuu wa jeshi lake, walikuwa wamelala; Sauli alikuwa amelala ndani ya kambi akiwa amezungukwa na wanajeshi. 6 Kisha Daudi akamuuliza hivi Ahimeleki Mhiti+ na Abishai+ mwana wa Seruya,+ ndugu ya Yoabu: “Ni nani atakayeshuka pamoja nami kwenda kwa Sauli kambini?” Abishai akajibu: “Mimi nitashuka pamoja nawe.” 7 Basi Daudi na Abishai wakaenda kwa jeshi hilo usiku, wakamkuta Sauli amelala ndani ya kambi mkuki wake ukiwa umedungwa ardhini karibu na kichwa chake; Abneri na wanajeshi walikuwa wamelala kumzunguka Sauli.

8 Ndipo Abishai akamwambia Daudi: “Leo Mungu amemtia adui yako mikononi mwako.+ Na sasa tafadhali, acha nimpigilie ardhini kwa mkuki mara moja tu, wala sitafanya hivyo mara mbili.” 9 Hata hivyo, Daudi akamwambia Abishai: “Usimdhuru, kwa maana ni nani anayeweza kuinua mkono wake dhidi ya mtiwa-mafuta wa Yehova+ na asiwe na hatia?”+ 10 Daudi akaendelea kusema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, Yehova mwenyewe atampiga,+ au siku yake itafika+ naye atakufa, au ataenda vitani na kuuawa.+ 11 Ni jambo nisiloweza kamwe kuwazia, kulingana na maoni ya Yehova, kwamba niinue mkono wangu dhidi ya mtiwa-mafuta wa Yehova!+ Sasa, tafadhali, chukua huo mkuki ulio karibu na kichwa chake na hilo gudulia la maji, twende zetu.” 12 Basi Daudi akachukua mkuki na gudulia la maji karibu na kichwa cha Sauli, wakaenda zao. Hakuna yeyote aliyejua wala kuwaona+ wala kuamka, kwa maana wote walikuwa wamelala, kwa sababu walikuwa wameshikwa na usingizi mzito kutoka kwa Yehova. 13 Kisha Daudi akavuka ng’ambo na kusimama juu ya mlima uliokuwa umbali fulani kutoka kwenye kambi ya Sauli.

14 Daudi akawaita kwa sauti wanajeshi hao na Abneri+ mwana wa Neri, akisema: “Abneri, unanisikia?” Abneri akajibu: “Wewe ni nani unayemwita mfalme?” 15 Daudi akamwambia Abneri: “Je, wewe si mwanamume? Na ni nani aliye kama wewe katika Israeli? Kwa nini basi hukumlinda bwana wako mfalme? Kwa sababu mwanajeshi mmoja aliingia kambini ili kumwangamiza bwana wako mfalme.+ 16 Jambo ulilofanya si zuri. Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, mnastahili kufa, kwa sababu hamkuendelea kumlinda bwana wenu, mtiwa-mafuta wa Yehova.+ Sasa angalia kila mahali! Uko wapi mkuki wa mfalme na gudulia la maji+ lililokuwa karibu na kichwa chake?”

17 Ndipo Sauli akaitambua sauti ya Daudi na kumuuliza: “Je, hiyo ni sauti yako mwanangu Daudi?”+ Daudi akajibu: “Ni sauti yangu, bwana wangu mfalme.” 18 Halafu akaendelea kusema: “Bwana wangu kwa nini unanifuatia mimi mtumishi wako,+ nimefanya nini, nami nina hatia ya kosa gani?+ 19 Tafadhali, bwana wangu mfalme, yasikilize maneno yangu mimi mtumishi wako: Ikiwa ni Yehova aliyekuchochea dhidi yangu, acha akubali* toleo langu la nafaka. Lakini ikiwa ni wanadamu wamekuchochea,+ wamelaaniwa mbele za Yehova, kwa sababu leo wamenifukuza ili nisiungane na urithi wa Yehova,+ wakisema, ‘Nenda, abudu miungu mingine!’ 20 Na sasa usiache damu yangu imwagike ardhini mbali kutoka mbele za* Yehova, kwa maana mfalme wa Israeli ametoka kwenda kutafuta kiroboto mmoja,+ kama mtu anayewinda kware milimani.”

21 Ndipo Sauli akasema: “Nimetenda dhambi.+ Rudi, mwanangu Daudi, kwa maana sitakudhuru tena, kwa sababu umeona uhai wangu kuwa wenye* thamani+ leo. Naam, nimetenda kipumbavu, nami nimekosea sana.” 22 Daudi akamwambia: “Mkuki wa mfalme ndio huu. Mruhusu mmoja wa vijana wako aje kuuchukua. 23 Yehova ndiye atakayemlipa kila mtu kulingana na uadilifu wake mwenyewe+ na uaminifu wake mwenyewe, kwa kuwa leo Yehova alikutia mikononi mwangu, lakini sikutaka kuinua mkono wangu dhidi ya mtiwa-mafuta wa Yehova.+ 24 Tazama! Kama nilivyoona uhai wako kuwa wenye* thamani leo, uhai wangu na uwe wenye* thamani machoni pa Yehova, na aniokoe kutoka katika mateso yote.”+ 25 Sauli akamwambia Daudi: “Ubarikiwe, mwanangu Daudi. Hakika utatenda mambo makubwa, na hakika utashinda.”+ Kisha Daudi akaenda zake, na Sauli akarudi kwake.+

27 Hata hivyo, Daudi akasema moyoni mwake: “Siku moja mkono wa Sauli utaniua. Jambo bora la kufanya ni kukimbilia+ nchi ya Wafilisti; halafu Sauli atakata tamaa ya kunitafuta katika eneo lote la Israeli,+ nami nitaponyoka kutoka mkononi mwake.” 2 Basi Daudi akaondoka pamoja na wanaume 600+ waliokuwa naye, akavuka kwenda kwa Akishi+ mwana wa Maoki, mfalme wa Gathi. 3 Daudi na wanaume wake wakakaa na Akishi huko Gathi, kila mwanamume na familia yake. Daudi alikuwa na wake zake wawili, Ahinoamu+ wa Yezreeli na Abigaili+ Mkarmeli, mjane wa Nabali. 4 Sauli alipoambiwa kwamba Daudi alikuwa amekimbia kwenda Gathi, aliacha kumtafuta.+

5 Ndipo Daudi akamwambia Akishi: “Ikiwa nimepata kibali machoni pako, naomba unipe mahali katika mojawapo ya majiji ya mashambani, ili niishi huko. Kwa nini mimi mtumishi wako niishi pamoja nawe katika jiji hili la kifalme?” 6 Basi Akishi akampa Siklagi+ siku hiyo. Ndiyo sababu tangu siku hiyo Siklagi limekuwa jiji la wafalme wa Yuda.

7 Daudi aliishi katika eneo la mashambani la Wafilisti kwa muda wa mwaka mmoja na miezi minne.+ 8 Daudi alikuwa akipanda pamoja na wanaume wake kuwavamia Wageshuri,+ Wagirzi, na Waamaleki,+ kwa maana walikuwa wakikaa katika nchi iliyoanzia Telamu mpaka Shuri+ na kushuka mpaka nchi ya Misri. 9 Daudi alipokuwa akiishambulia nchi, hakumwacha hai mwanamume wala mwanamke yeyote,+ bali alichukua kondoo, ng’ombe, punda, ngamia, na mavazi, kisha alirudi kwa Akishi. 10 Na Akishi alipokuwa akimuuliza: “Ulivamia wapi leo?” Daudi alimjibu: “Upande wa kusini wa* Yuda”+ au “Upande wa kusini wa Wayerahmeeli”+ au “Upande wa kusini wa Wakeni.”+ 11 Daudi hakumwacha hai mwanamume au mwanamke yeyote ili wasiletwe Gathi, kwa kuwa alisema: “Wasije wakawaambia habari zetu wakisema, ‘Hivi ndivyo Daudi alivyofanya.’” (Alizoea kufanya hivyo muda wote alioishi katika eneo la mashambani la Wafilisti.) 12 Kwa hiyo Akishi akamwamini Daudi akisema moyoni mwake: “Bila shaka ananuka miongoni mwa watu wake wa Israeli, kwa hiyo atakuwa mtumishi wangu sikuzote.”

28 Siku hizo Wafilisti walikusanya majeshi yao kwenda kupigana vita na Waisraeli.+ Basi Akishi akamwambia Daudi: “Bila shaka unajua kwamba wewe na wanaume wako mtaenda pamoja nami vitani.”+ 2 Kwa hiyo Daudi akamwambia Akishi: “Kwa hakika unajua jambo ambalo mimi mtumishi wako nitafanya.” Akishi akamwambia Daudi: “Ndiyo sababu nitakuweka kuwa mlinzi wangu wa kudumu.”*+

3 Wakati huo Samweli alikuwa amekufa, na Waisraeli wote walikuwa wamemwombolezea na kumzika katika jiji lake mwenyewe la Rama.+ Naye Sauli alikuwa amewaondoa nchini watu wanaowasiliana na roho na pia wabashiri.+

4 Wafilisti wakakusanyika na kwenda kupiga kambi Shunemu.+ Basi Sauli akawakusanya Waisraeli wote, nao wakapiga kambi Gilboa.+ 5 Sauli alipoona kambi ya Wafilisti, akaogopa, na moyo wake ukatetemeka sana.+ 6 Ingawa Sauli alikuwa akimwomba Yehova ushauri,+ Yehova hakumjibu kamwe, iwe ni katika ndoto au kwa Urimu+ au kupitia manabii. 7 Hatimaye Sauli akawaambia watumishi wake: “Nitafutieni mwanamke anayewasiliana na roho,+ nitaenda kwake kumwomba ushauri.” Watumishi wake wakamwambia: “Tazama! Kuna mwanamke anayewasiliana na roho kule En-dori.”+

8 Kwa hiyo Sauli akaficha sura yake, akavaa mavazi mengine na kwenda kwa mwanamke huyo usiku akiwa na wanaume wake wawili. Akasema: “Tafadhali, nifanyie uaguzi* kwa kuwasiliana na roho,+ nipandishie yule nitakayekutajia.” 9 Hata hivyo, mwanamke huyo akamwambia: “Unajua vizuri mambo ambayo Sauli alifanya, jinsi alivyowaondoa nchini watu wanaowasiliana na roho na pia wabashiri.+ Kwa nini basi unajaribu kunitega ili niuawe?”+ 10 Ndipo Sauli akamwapia kwa jina la Yehova, akisema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, hutakuwa na hatia yoyote kuhusu jambo hili!” 11 Basi mwanamke huyo akamuuliza: “Nikupandishie nani?” Akajibu: “Nipandishie Samweli.” 12 Mwanamke huyo alipomwona “Samweli,”*+ akapiga kelele kwa sauti yake yote na kumwambia Sauli: “Kwa nini ulinidanganya? Wewe ni Sauli!” 13 Mfalme akamwambia: “Usiogope, lakini unaona nini?” Mwanamke huyo akamjibu Sauli: “Ninaona mtu fulani kama mungu akipanda kutoka duniani.” 14 Mara moja Sauli akamuuliza mwanamke huyo: “Yukoje?” akamwambia: “Ni mwanamume mzee anayepanda, amevaa joho lisilo na mikono.”+ Ndipo Sauli akatambua kwamba ni “Samweli,” naye akainama chini kifudifudi na kusujudu.

15 Kisha “Samweli” akamuuliza Sauli: “Kwa nini umenisumbua kwa kufanya nipandishwe?” Sauli akamjibu: “Niko katika taabu kubwa. Wafilisti wanapigana nami, na Mungu ameniacha, hanijibu tena, iwe ni kupitia manabii au katika ndoto;+ ndiyo sababu nimekuita uniambie ninalopaswa kufanya.”+

16 “Samweli” akamuuliza: “Kwa nini unaniomba ushauri wakati ambapo Yehova amekuacha+ na kuwa adui yako? 17 Yehova atajifanyia mwenyewe yale aliyotabiri kupitia mimi: Yehova ataurarua ufalme kutoka mikononi mwako na kumpa mwenzako, Daudi.+ 18 Kwa sababu hukuitii sauti ya Yehova, nawe hukutekeleza hasira yake kali dhidi ya Waamaleki,+ ndiyo sababu Yehova anakutendea mambo haya leo. 19 Pia, Yehova atakutia wewe pamoja na Waisraeli mikononi mwa Wafilisti,+ na kesho wewe+ na wana wako+ mtakuwa pamoja nami. Yehova atalitia pia jeshi la Israeli mikononi mwa Wafilisti.”+

20 Papo hapo Sauli akaanguka chini akiwa amenyooka mwili mzima naye akaogopa sana kwa sababu ya maneno ya “Samweli.” Nguvu zikamwishia, kwa sababu hakuwa amekula chakula mchana wote na usiku kucha. 21 Mwanamke huyo alipomkaribia Sauli na kuona kwamba ana wasiwasi mwingi, akamwambia: “Mimi kijakazi wako nimetii jambo ulilosema, na nimehatarisha uhai wangu*+ kwa kufanya uliloniambia nifanye. 22 Sasa, tafadhali, sikiliza maneno ninayotaka kukwambia mimi mtumishi wako. Acha nikuandalie kipande cha mkate, ule ili upate nguvu za kuendelea na safari.” 23 Lakini akakataa na kusema: “Sitakula.” Hata hivyo, watumishi wake na pia mwanamke huyo wakaendelea kumsihi ale. Mwishowe akawasikiliza, akainuka kutoka ardhini na kuketi kitandani. 24 Mwanamke huyo alikuwa na ndama aliyenona nyumbani mwake, basi akamchinja* haraka, akachukua unga, akaukanda na kuoka mikate isiyo na chachu. 25 Akamwandalia Sauli na watumishi wake, nao wakala. Kisha wakaondoka na kwenda zao usiku huo.+

29 Wafilisti+ walikusanya majeshi yao yote kule Afeki Waisraeli walipokuwa wakipiga kambi karibu na chemchemi huko Yezreeli.+ 2 Na watawala wa Wafilisti walikuwa wakipita wakiwa na vikosi vyao vya mamia na maelfu, naye Daudi na wanaume wake walikuwa wakiwafuata nyuma wakiwa na Akishi.+ 3 Lakini wakuu wa Wafilisti wakauliza: “Waebrania hawa wamekuja kufanya nini?” Akishi akawajibu hivi wakuu wa Wafilisti: “Huyu ni Daudi, mtumishi wa Mfalme Sauli wa Israeli, naye ameishi pamoja nami kwa mwaka mmoja au zaidi.+ Tangu siku aliyokimbilia kwangu mpaka leo sijampata na kosa lolote.” 4 Lakini wakuu wa Wafilisti wakamkasirikia vikali Akishi na kumwambia: “Mrudishe mtu huyu.+ Acha arudi mahali ulipompa. Usimruhusu ashuke kwenda pamoja nasi vitani, asije akatugeuka na kutushambulia wakati wa vita.+ Kuna njia gani bora ya mtu huyu kupata kibali cha bwana wake isipokuwa kumpelekea vichwa vya wanaume wetu? 5 Je, huyu si Daudi waliyeimba kumhusu walipocheza dansi, wakisema:

‘Sauli ameua maelfu yake,

Na Daudi makumi yake ya maelfu’?”+

6 Basi Akishi+ akamwita Daudi na kumwambia: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, wewe ni mnyoofu, nami ningependa uende vitani pamoja na jeshi langu,+ kwa sababu tangu siku uliyokuja kwangu mpaka leo sijakupata na kosa lolote.+ Lakini watawala hawakuamini.+ 7 Hivyo rudi kwa amani, na usifanye jambo lolote ambalo halitawapendeza watawala wa Wafilisti.” 8 Lakini Daudi akamuuliza Akishi: “Kwa nini? Nimefanya nini? Ni kosa gani ambalo umenipata nalo mimi mtumishi wako tangu siku niliyokuja kwako mpaka leo? Kwa nini nisiende pamoja nawe kupigana na maadui wako, bwana wangu mfalme?” 9 Akishi akamjibu hivi Daudi: “Kwa maoni yangu, umekuwa mwema kama malaika wa Mungu.+ Lakini wakuu wa Wafilisti wamesema, ‘Usimruhusu apande pamoja nasi kwenda vitani.’ 10 Sasa amka asubuhi na mapema pamoja na watumishi wa bwana wako waliokuja nawe; amkeni na kuondoka asubuhi na mapema mara tu kutakapopambazuka.”

11 Basi Daudi na wanaume wake wakaamka asubuhi na mapema ili warudi katika nchi ya Wafilisti, nao Wafilisti wakapanda kwenda Yezreeli.+

30 Daudi na wanaume wake walipofika Siklagi+ siku ya tatu, Waamaleki+ walikuwa wamevamia upande wa kusini* na pia Siklagi, nao walikuwa wameshambulia Siklagi na kuliteketeza kwa moto. 2 Walikuwa wamewateka wanawake+ na watu wote waliokuwa humo, kuanzia mdogo zaidi mpaka mkubwa zaidi. Hawakumuua yeyote, lakini waliwachukua na kwenda zao. 3 Daudi na wanaume wake walipofika jijini, walikuta jiji lote limeteketezwa, na wake zao na wana wao na mabinti wao walikuwa wamechukuliwa mateka. 4 Basi Daudi na wanaume waliokuwa pamoja naye wakaanza kulia kwa sauti kubwa mpaka wakakosa nguvu za kuendelea kulia. 5 Wake wawili wa Daudi walikuwa pia wametekwa, Ahinoamu wa Yezreeli na Abigaili mjane wa Nabali Mkarmeli.+ 6 Daudi alifadhaika sana, kwa sababu wanaume wake walitaka kumpiga mawe, kwa maana wanaume wote walikuwa na uchungu mwingi sana kwa kuwapoteza wana na mabinti wao. Lakini Daudi akajitia nguvu kwa msaada wa Yehova Mungu wake.+

7 Kisha Daudi akamwambia kuhani Abiathari,+ mwana wa Ahimeleki: “Tafadhali ilete ile efodi hapa.”+ Kwa hiyo Abiathari akamletea Daudi hiyo efodi. 8 Daudi akamuuliza Yehova:+ “Je, nilifuatie kundi hili la wavamizi? Je, nitawafikia?” Ndipo Akamwambia: “Wafuatie, kwa maana hakika utawafikia, nawe utawaokoa waliotekwa.”+

9 Mara moja Daudi akaondoka na wanaume 600+ waliokuwa pamoja naye, wakaenda mpaka kwenye Korongo* la Besori, na wanaume kadhaa wakabaki hapo. 10 Daudi akaendelea kuwafuatia akiwa na wanaume 400, lakini wanaume 200 waliokuwa wamechoka sana wasiweze kuvuka Korongo la Besori wakabaki hapo.+

11 Wanaume hao wakamkuta mwanamume fulani Mmisri mbugani na kumpeleka kwa Daudi. Wakampa chakula na maji ya kunywa, 12 na pia kipande cha keki ya tini zilizoshinikizwa na keki mbili za zabibu kavu. Baada ya kula, akapata nguvu,* kwa sababu hakuwa amekula chakula chochote wala kunywa maji kwa siku tatu, mchana na usiku. 13 Sasa Daudi akamuuliza: “Wewe ni mtumishi wa nani, na unatoka wapi?” akajibu: “Mimi ni mtumishi Mmisri, mtumwa wa Mwamaleki fulani, lakini bwana wangu aliniacha kwa sababu nilishikwa na ugonjwa siku tatu zilizopita. 14 Tulivamia upande wa kusini wa* Wakerethi+ na eneo la Yuda na upande wa kusini wa* Kalebu,+ nasi tukateketeza Siklagi kwa moto.” 15 Daudi akamuuliza: “Je, utaniongoza chini kwenye kundi hilo la wavamizi?” Akajibu: “Ukiniapia mbele za Mungu kwamba hutaniua wala kunitia mikononi mwa bwana wangu, nitakuongoza chini kwenye kundi hilo la wavamizi.”

16 Basi akamwongoza chini mahali walipokuwa wameenea kotekote, wakila na kunywa na kusherehekea kwa sababu ya nyara nyingi sana walizokuwa wamechukua kutoka katika nchi ya Wafilisti na nchi ya Yuda. 17 Kisha Daudi akawaua kuanzia asubuhi kabla ya mapambazuko mpaka jioni siku iliyofuata; hakuna mtu yeyote aliyeponyoka+ isipokuwa wanaume 400 waliopanda ngamia na kukimbia. 18 Daudi akapata vitu vyote ambavyo Waamaleki walikuwa wamechukua,+ naye akawaokoa wake zake wawili. 19 Hawakukosa kitu chochote kilichokuwa chao, kuanzia kidogo zaidi mpaka kikubwa zaidi. Waliwapata wana na mabinti wao na kuchukua nyara;+ Daudi alipata kila kitu walichochukua. 20 Basi Daudi akachukua makundi yote ya kondoo na ng’ombe, nao wakawatanguliza wanyama hao mbele ya mifugo yao wenyewe. Wakasema: “Hizi ni nyara za Daudi.”

21 Kisha Daudi akafika kwa wale wanaume 200 waliobaki kwenye Korongo la Besori+ kwa sababu walikuwa wamechoka sana wasiweze kwenda naye, nao wakaja kumpokea Daudi na watu waliokuwa pamoja naye. Daudi alipofika karibu na wanaume hao, akawajulia hali. 22 Hata hivyo, kila mtu mbaya na asiyefaa kitu kati ya watu walioenda na Daudi akasema: “Kwa kuwa hawakwenda pamoja nasi, hatutawapa nyara yoyote tuliyochukua, lakini kila mmoja wao anaweza kumchukua mke wake na wanawe na kwenda zake.” 23 Hata hivyo, Daudi akasema: “Msifanye hivyo ndugu zangu kuhusiana na vitu ambavyo Yehova ametupatia. Alitulinda na kulitia mikononi mwetu kundi la wavamizi lililokuja kutuvamia.+ 24 Ni nani atakayekubaliana nanyi katika jambo hili? Fungu la yule aliyeshuka kwenda vitani litakuwa sawa na fungu la yule aliyeketi kando ya mizigo.+ Wote watapata fungu lilelile.”+ 25 Na kuanzia siku hiyo na kuendelea, akalifanya jambo hilo kuwa sheria na amri katika Israeli mpaka leo hii.

26 Daudi aliporudi Siklagi, aliwapelekea wazee wa Yuda waliokuwa rafiki zake baadhi ya nyara hizo, akisema: “Hii ni zawadi* yenu kutoka katika nyara za maadui wa Yehova.” 27 Alizipeleka kwa wale waliokuwa Betheli,+ kwa wale waliokuwa Ramothi la Negebu,* kwa wale waliokuwa Yatiri,+ 28 kwa wale waliokuwa Aroeri, kwa wale waliokuwa Sifmothi, kwa wale waliokuwa Eshtemoa,+ 29 kwa wale waliokuwa Rakali, kwa wale waliokuwa katika majiji ya Wayerahmeeli,+ kwa wale waliokuwa katika majiji ya Wakeni,+ 30 kwa wale waliokuwa Horma,+ kwa wale waliokuwa Borashani, kwa wale waliokuwa Athaki, 31 kwa wale waliokuwa Hebroni,+ na sehemu zote ambazo Daudi na wanaume wake walitembelea kwa ukawaida.

31 Sasa Wafilisti walikuwa wakipigana na Waisraeli.+ Na wanaume wa Israeli wakawakimbia Wafilisti, na wengi wakauawa kwenye Mlima Gilboa.+ 2 Wafilisti wakamkaribia sana Sauli na wanawe, nao wakamuua Yonathani,+ Abinadabu, na Malki-shua, wana wa Sauli.+ 3 Vita vikawa vikali sana dhidi ya Sauli, na wapiga mishale wakampata na kumjeruhi vibaya.+ 4 Ndipo Sauli akamwambia mtu aliyembebea silaha: “Chomoa upanga wako unichome nao, ili watu hawa wasiotahiriwa+ wasije kunichoma kwa upanga na kunitendea kikatili.”* Lakini mtu huyo aliyembebea silaha hakutaka kufanya hivyo, kwa sababu aliogopa sana. Basi Sauli akachukua upanga na kuuangukia.+ 5 Mtu aliyembebea silaha alipoona kwamba Sauli amekufa,+ yeye pia akauangukia upanga wake mwenyewe, akafa pamoja naye. 6 Basi Sauli, wanawe watatu, mtu aliyembebea silaha, na wanaume wake wote wakafa pamoja siku hiyo.+ 7 Watu wa Israeli waliokuwa katika eneo la bondeni na katika eneo la Yordani walipoona kwamba wanaume wa Israeli wamekimbia na kwamba Sauli na wanawe wamekufa, wakaanza kuyaacha majiji na kukimbia;+ kisha Wafilisti wakaja na kukaa humo.

8 Siku iliyofuata, Wafilisti walipokuja kuwavua waliouawa vitu walivyokuwa navyo, walimkuta Sauli na wanawe watatu wakiwa wameanguka kwenye Mlima Gilboa.+ 9 Basi wakamkata kichwa na kumvua silaha zake na kutuma ujumbe kotekote katika nchi ya Wafilisti ili habari+ zienezwe katika nyumba za* sanamu zao+ na miongoni mwa watu. 10 Kisha wakaweka silaha zake katika nyumba ya sanamu za Ashtorethi na kuitundika maiti yake kwenye ukuta wa Beth-shani.+ 11 Wakaaji wa Yabeshi-gileadi+ waliposikia mambo ambayo Wafilisti walikuwa wamemtendea Sauli, 12 mashujaa wote wakaondoka na kusafiri usiku kucha, wakaondoa maiti za Sauli na wanawe kutoka kwenye ukuta wa Beth-shani. Wakarudi Yabeshi na kuzichoma moto huko. 13 Kisha wakachukua mifupa yao+ na kuizika chini ya mti wa mwesheli huko Yabeshi,+ nao wakafunga kwa siku saba.

Au “kutoka Rama, Msufu.”

Au “kumwinamia.”

Tnn., “alikuwa amefunga tumbo lake la uzazi.”

Au “na kwa nini moyo wako unahisi vibaya?”

Yaani, hema la ibada.

Au “uchungu nafsini.”

Au “mwanamke aliyefadhaika sana rohoni.”

Angalia Kamusi.

Au “akamwelekezea fikira.”

Au labda, “Wakati unaofaa ulipofika.”

Maana yake “Jina la Mungu.”

Tnn., “lililo jema machoni pako.”

Efa ilikuwa sawa na lita 22 au kilogramu 13 hivi. Angalia Nyongeza B14.

Au “Kwa uhai wa nafsi yako.”

Inaonekana ni Elkana.

Au “Nguvu zangu zimekwezwa.” Angalia Kamusi.

Tnn., “amedhoofika.”

Au “huhuisha.”

Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.

Au labda, “jaa la takataka; jalalani.”

Au labda, “Wale wanaoshindana na Yehova wataogopeshwa.”

Au “nguvu za.” Angalia Kamusi.

Au “alikuwa akimtumikia.”

Au “ambacho nafsi yako inatamani.”

Tnn., “amefungwa.”

Au labda, “Mungu atakuwa mpatanishi wake.”

Au labda, “kufanya moshi wa dhabihu upae juu.”

Tnn., “wana wa Israeli.”

Tnn., “mnapiga teke.”

Tnn., “mkono wenu na wa.”

Au “kilicho katika moyo wangu na nafsi yangu.”

Yaani, hema la ibada.

Tnn., “lianguke ardhini.”

Tnn., “Kwa nini Yehova ametushinda leo kwa kuwatumia Wafilisti?”

Au labda, “katikati ya.”

Au “wala kutia moyoni jambo hilo.”

Maana yake “Utukufu uko Wapi?”

Au “hekalu la.”

Tnn., “Ni Dagoni tu aliyebaki.”

Tnn., “ulikuwa mzito dhidi ya.”

Au “ugonjwa wa puru.”

Tnn., “wanaume 70, wanaume 50,000.”

Au “kuomboleza mbele za.”

Maana yake “Jiwe la Msaada.”

Au “wachanganyaji wa manukato.”

Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.

Tnn., “amefunua sikio la.”

Au “atakayewazuia watu wangu wasipite mipaka.”

Tnn., “mambo yote yaliyo moyoni mwako.”

Yaani, methali.

Au “koo zenu.”

Tnn., “Naye alikuwa kama bubu.”

Au “makubaliano.”

Tnn., “kama mtu mmoja.”

Yaani, kuanzia saa 8 hivi usiku hadi saa 12 asubuhi.

Tnn., “nimesikiliza sauti yenu kuhusiana na.”

Tnn., “anayetembea mbele yenu.”

Tnn., “ili inifanye nitazame upande mwingine.”

Tnn., “hamkupata chochote mkononi mwangu.”

Au “vya kuwaziwa.”

Au “vya kuwaziwa.”

Au “kwa unyoofu.”

Hati ya Kiebrania haionyeshi idadi ya miaka yake.

Au “tarumbeta.”

Au “sijautuliza uso wa.”

Kipimo cha zamani ambacho ni karibu theluthi mbili za shekeli.

Tnn., “kituo cha ulinzi cha.”

Yaani, eneo linaloweza kulimwa kwa plau na ng’ombe dume wawili katika siku moja.

Tnn., “siku hiyo.”

Tnn., “Rudisha mkono wako.”

Tnn., “mkate wowote.”

Tnn., “nchi yote ikafika.”

Au “wokovu.”

Tnn., “wakamkomboa.”

Au “Usiwahurumie.”

Au “walimhurumia.”

Au “Ninahuzunika.”

Au “waliwahurumia.”

Au “ubashiri.”

Tnn., “sanamu za terafimu,” yaani, miungu ya familia; sanamu.

Au “hataghairi.”

Au “aghairi.”

Au labda, “kwa ujasiri.”

Tnn., “uchungu wa kifo umepita.”

Tnn., “kambi zao.”

Tnn., “Nchi Tambarare ya Chini ya.”

Alikuwa na urefu wa mita 2.9 hivi (futi 9 na inchi 5.75). Angalia Nyongeza B14.

Karibu kilogramu 57. Angalia Nyongeza B14.

Karibu kilogramu 6.84. Angalia Nyongeza B14.

Au “Nataka kushindana na.”

Efa ilikuwa sawa na lita 22 au kilogramu 13 hivi. Angalia Nyongeza B14.

Tnn., “maziwa.”

Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”

Au “kushindana na.”

Au “ashindane na.”

Au “asiogope.”

Au “mwanamume wa vita.”

Au “utaya wake.” Tnn., “ndevu zake.”

Au “ameshindana na.”

Au “umeshindana naye.”

Tnn., “Na kutaniko hili lote litajua.”

Au “Kama nafsi yako inavyoishi.”

Au “nafsi ya Yonathani ikashikamana na nafsi ya Daudi.”

Au “kama nafsi yake mwenyewe.”

Au “kama nafsi yake mwenyewe.”

Au “alitenda kwa hekima.”

Au “kutenda kama nabii.”

Yaani, Sauli.

Tnn., “akitoka nje na kuingia mbele ya watu.”

Au “kutenda kwa hekima.”

Au “Nitakuwa baba mkwe wako.”

Au “alivyozidi kutenda kwa hekima.”

Au “Aliitia nafsi yake mikononi mwake.”

Au “wokovu.”

Au “mungu wa familia; sanamu.”

Au “mungu wa familia; sanamu.”

Au “akiwa na mavazi machache.”

Au “nafsi yako inavyoishi.”

Au “kama nafsi yake mwenyewe.”

Tnn., “siku ya kazi.”

Tnn., “kwa aibu ya uchi wa mama yako?”

Tnn., “kwa maana yeye ni mwana wa kifo.”

Tnn., “mbegu yangu.”

Tnn., “mbegu yako.”

Au “hawajafanya ngono.”

Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”

Tnn., “mikononi mwao.”

Au “waliokuwa na uchungu nafsini.”

Au “aliye mwaminifu.”

Tnn., “wakimbiaji.”

Au “kila nafsi.”

Au “nafsi yako.”

Au “nafsi yangu.”

Tnn., “amemuuza mikononi mwangu.”

Au labda, “wamiliki wa mashamba.”

Au labda, “Daudi aliogopa kwa sababu.”

Au “alikuwa akiitafuta nafsi yake.”

Tnn., “akauimarisha mkono wake.”

Tnn., “upande wa kulia.”

Au labda, “wa jangwa; nyika.”

Au “koo zote za.”

Tnn., “afunike miguu yake.”

Au “dhamiri ya Daudi ikaendelea kumchoma.”

Au labda, “akawatawanya.”

Au “kuiua nafsi yangu.”

Tnn., “mbegu yangu.”

Jiji fulani kule Yuda; si Mlima Karmeli.

Au “utambuzi.”

Tnn., “siku nzuri.”

Au “asiye na maana.”

Sea moja ilikuwa sawa na lita 7.33 (vibaba 6.66). Angalia Nyongeza B14.

Au labda, “Mungu na amwadhibu Daudi, tena vikali.”

Tnn., “mtu yeyote anayekojoa ukutani.” Huu ni msemo wa Kiebrania wa kuwadharau wanaume.

Maana yake “Mpumbavu; Mjinga.”

Au “usiokoe.”

Tnn., “baraka.”

Au “kutafuta nafsi yako.”

Au “nafsi yako.”

Au “kuokoa.”

Au “nisiokoe.”

Tnn., “mtu yeyote anayekojoa ukutani.” Huu ni msemo wa Kiebrania wa kuwadharau wanaume.

Tnn., “moyo wa Nabali ulikuwa umechangamka sana.”

Tnn., “amerudisha uovu wa Nabali juu ya kichwa chake mwenyewe!”

Au labda, “jangwa; nyika.”

Tnn., “anuse.”

Au “kutoka kwenye uwepo wa.”

Au “umeona nafsi yangu kuwa yenye.”

Au “nafsi yako kuwa yenye.”

Au “nafsi yangu na iwe yenye.”

Au “Dhidi ya Negebu ya.”

Tnn., “kuwa mlinzi wa kichwa changu siku zote.”

Au “nibashirie.”

Au “mtu aliyeonekana kama Samweli.”

Au “nimetia nafsi yangu mikononi mwangu.”

Au “akamtoa dhabihu.”

Au “Negebu.”

Angalia Kamusi.

Tnn., “roho yake ikamrudia.”

Au “Negebu ya.”

Au “Negebu ya.”

Tnn., “baraka.”

Tnn., “la kusini.”

Au “na kunitesa.”

Au “mahekalu ya.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki