Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt 2 Samweli 1:1-24:25
  • 2 Samweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • 2 Samweli
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
2 Samweli

KITABU CHA PILI CHA SAMWELI

1 Baada ya kifo cha Sauli, Daudi aliporudi baada ya kuwashinda* Waamaleki, alikaa Siklagi+ kwa siku mbili. 2 Siku ya tatu, mtu fulani alikuja kutoka katika kambi ya Sauli akiwa amevaa nguo zilizoraruka, na akiwa na mavumbi kichwani. Alipomkaribia Daudi, alijiangusha chini na kumwinamia.

3 Daudi akamuuliza: “Umetoka wapi?” Akajibu: “Nimetoroka katika kambi ya Israeli.” 4 Daudi akamuuliza: “Ni nini kilichotokea? Tafadhali niambie.” Akamwambia: “Watu wamekimbia kutoka vitani na wengi wameanguka na kufa. Hata Sauli na Yonathani mwanawe wamekufa.”+ 5 Kisha Daudi akamuuliza hivi kijana huyo aliyemletea habari: “Unajuaje kwamba Sauli na Yonathani mwanawe wamekufa?” 6 Kijana huyo akajibu: “Nilifika kwenye Mlima Gilboa+ bila kutazamia, nikamwona Sauli akiwa ameegemea mkuki wake, na magari ya vita na wapanda farasi walikuwa wamemfikia.+ 7 Alipogeuka na kuniona, aliniita, nami nikasema, ‘Naam!’ 8 Akaniuliza, ‘Wewe ni nani?’ nikajibu, ‘Mimi ni Mwamaleki.’+ 9 Kisha akasema, ‘Tafadhali, nikaribie uniue, kwa maana nina maumivu makali sana, lakini bado niko hai.’ 10 Basi nikamkaribia na kumuua,+ kwa maana nilijua kwamba hangeendelea kuishi baada ya kuanguka chini akiwa amejeruhiwa. Kisha nikachukua taji lililokuwa kichwani mwake na kikuku kilichokuwa mkononi mwake, nami nimevileta hapa kwako bwana wangu.”

11 Ndipo Daudi akashika mavazi yake na kuyararua, na watu wote waliokuwa pamoja naye wakafanya vivyo hivyo. 12 Nao wakaomboleza na kulia na kufunga+ mpaka jioni kwa ajili ya Sauli, kwa ajili ya Yonathani mwanawe, kwa ajili ya watu wa Yehova, kwa ajili ya nyumba ya Israeli,+ kwa sababu walikuwa wameuawa kwa upanga.

13 Daudi akamuuliza hivi kijana aliyemletea habari: “Unatoka wapi?” Akajibu: “Mimi ni mwana wa mkaaji mgeni, Mwamaleki.” 14 Kisha Daudi akamuuliza: “Kwa nini hukuogopa kuinua mkono wako kumuua mtiwa-mafuta wa Yehova?”+ 15 Ndipo Daudi akamwita kijana mmoja na kumwambia: “Njoo umuue.” Basi akampiga na kumuua.+ 16 Daudi akamwambia: “Damu yako na iwe juu ya kichwa chako mwenyewe, kwa sababu kinywa chako mwenyewe kilitoa ushahidi dhidi yako, uliposema, ‘Mimi mwenyewe nilimuua mtiwa-mafuta wa Yehova.’”+

17 Kisha Daudi akaimba wimbo huu wa maombolezo kwa ajili ya Sauli na Yonathani mwanawe+ 18 na kusema kwamba watu wa Yuda wafundishwe wimbo wa maombolezo unaoitwa “Upinde,” ulioandikwa katika kitabu cha Yashari:+

19 “Ee Israeli, uzuri umeuawa kwenye vilima vyako.+

Jinsi walivyoanguka wanaume wenye nguvu!

20 Msiseme jambo hilo kule Gathi;+

Msilitangaze katika barabara za Ashkeloni,

Mabinti wa Wafilisti wasije wakashangilia,

Mabinti wa watu wasiotahiriwa wasije wakafurahi.

21 Enyi milima ya Gilboa,+

Msipate umande wowote wala mvua yoyote,

Wala mashamba yanayozaa michango mitakatifu,+

Kwa sababu ngao ya wenye nguvu ilichafuliwa huko,

Sasa ngao ya Sauli haijatiwa mafuta.

22 Kutoka kwenye damu ya waliouawa, kutoka kwenye mafuta ya wenye nguvu,

Upinde wa Yonathani haukurudi nyuma,+

Na upanga wa Sauli haukurudi bila mafanikio.+

23 Sauli na Yonathani,+ watu waliopendwa na kuthaminiwa* walipokuwa hai,

Na katika kifo hawakutenganishwa.+

Walikuwa wepesi kuliko tai,+

Walikuwa wenye nguvu kuliko simba.+

24 Enyi mabinti wa Israeli, mlilieni Sauli,

Aliyewavisha nguo nyekundu na mapambo,

Aliyetia mapambo ya dhahabu kwenye nguo zenu.

25 Jinsi wenye nguvu walivyoanguka vitani!

Yonathani amelala akiwa ameuawa juu ya vilima vyenu!+

26 Nimehuzunika kwa ajili yako, ndugu yangu Yonathani;

Nilikupenda sana.+

Upendo wako kwangu ulikuwa mzuri sana kuliko upendo wa wanawake.+

27 Jinsi wenye nguvu walivyoanguka

Na silaha za vita kuangamia!”

2 Baadaye Daudi akamuuliza hivi Yehova:+ “Je, nipande kwenda katika mojawapo ya majiji ya Yuda?” Yehova akamwambia: “Panda uende.” Kisha Daudi akamuuliza: “Niende wapi?” Akajibu: “Hebroni.”+ 2 Basi Daudi akapanda kwenda huko na wake zake wawili, Ahinoamu+ wa Yezreeli na Abigaili+ mjane wa Nabali Mkarmeli. 3 Daudi akawachukua pia wanaume waliokuwa pamoja naye,+ kila mmoja na familia yake, nao wakakaa katika majiji yanayozunguka Hebroni. 4 Kisha wanaume wa Yuda wakaja, na huko wakamtia mafuta Daudi awe mfalme juu ya nyumba ya Yuda.+

Wakamwambia Daudi: “Watu wa Yabesh-gileadi ndio waliomzika Sauli.” 5 Basi Daudi akawatuma wajumbe kwa watu wa Yabesh-gileadi na kuwaambia: “Yehova na awabariki, kwa sababu mlimtendea bwana wenu, Sauli, kwa upendo mshikamanifu kwa kumzika.+ 6 Yehova na awatendee kwa upendo mshikamanifu na uaminifu. Mimi pia nitawatendea fadhili kwa sababu mmefanya jambo hili.+ 7 Sasa mikono yenu na iwe na nguvu, nanyi muwe jasiri kwa sababu bwana wenu Sauli amekufa, na nyumba ya Yuda imenitia mafuta niwe mfalme juu yao.”

8 Lakini Abneri+ mwana wa Neri mkuu wa jeshi la Sauli, alikuwa amemchukua Ish-boshethi,+ mwana wa Sauli, akamvusha mpaka Mahanaimu+ 9 na kumfanya kuwa mfalme wa Gileadi,+ wa Waashuri, Yezreeli,+ Efraimu,+ Benjamini, na juu ya Waisraeli wote. 10 Ish-boshethi, mwana wa Sauli, alikuwa na umri wa miaka 40 alipokuwa mfalme wa Israeli, naye alitawala kwa miaka miwili. Hata hivyo, nyumba ya Yuda ilimuunga mkono Daudi.+ 11 Muda ambao Daudi alikuwa mfalme huko Hebroni juu ya nyumba ya Yuda ulikuwa miaka saba na miezi sita.+

12 Baada ya muda Abneri mwana wa Neri na watumishi wa Ish-boshethi, mwana wa Sauli, wakatoka Mahanaimu+ na kwenda Gibeoni.+ 13 Yoabu+ mwana wa Seruya+ na watumishi wa Daudi wakaondoka pia na kukutana nao kwenye kidimbwi cha Gibeoni; kikundi kimoja kiliketi upande mmoja wa kidimbwi hicho na kikundi cha pili upande wa pili. 14 Hatimaye Abneri akamwambia hivi Yoabu: “Acha vijana wasimame na kupambana* mbele yetu.” Ndipo Yoabu akasema: “Acha wasimame.” 15 Basi wakasimama, wakahesabiwa na kuvuka, 12 wa Benjamini na Ish-boshethi mwana wa Sauli, na 12 kutoka kati ya watumishi wa Daudi. 16 Kila mmoja alimkamata mwenzake kichwani na kumchoma kwa upanga ubavuni, na wote wakaanguka pamoja. Basi mahali hapo huko Gibeoni pakaitwa Helkath-hasurimu.

17 Vita vikawa vikali sana siku hiyo, mwishowe Abneri na wanaume wa Israeli wakashindwa na watumishi wa Daudi. 18 Basi wana watatu wa Seruya+ walikuwa mahali hapo—Yoabu,+ Abishai,+ na Asaheli;+ naye Asaheli alikuwa na mbio sana* kama swala katika nchi tambarare. 19 Asaheli akamkimbiza Abneri, naye hakugeuka kulia wala kushoto alipokuwa akimkimbiza. 20 Abneri alipotazama nyuma, aliuliza: “Ni wewe Asaheli?” akajibu: “Naam, ni mimi.” 21 Ndipo Abneri akamwambia: “Nenda kulia au kushoto umkamate kijana mmoja na kuchukua vitu vyake.” Lakini Asaheli hakutaka kuacha kumkimbiza. 22 Basi Abneri akamwambia tena Asaheli: “Acha kunikimbiza. Kwa nini nikuue? Nitawezaje kumtazama usoni ndugu yako Yoabu?” 23 Lakini hakuacha kumkimbiza, basi Abneri akamchoma tumboni kwa ncha ya nyuma ya mkuki,+ na mkuki huo ukatokea mgongoni mwake; akaanguka na kufa papo hapo. Kila mtu aliyefika mahali ambapo Asaheli alianguka na kufa alisimama hapo kwa muda.

24 Kisha Yoabu na Abishai wakaenda kumfuatia Abneri. Jua lilipokuwa likitua, wakafika kwenye kilima cha Ama, kilicho ng’ambo ya Gia kwenye njia inayoelekea katika nyika ya Gibeoni. 25 Wabenjamini wakakusanyika huko na kumfuata Abneri, wakawa kundi moja, nao wakajiimarisha juu ya kilima fulani. 26 Kisha Abneri akamwita Yoabu na kumuuliza: “Je, upanga utaendelea kuangamiza* bila kukoma? Je, hujui kwamba mwisho utakuwa mchungu tu? Basi, utangoja kwa muda gani ndipo uwaambie watu waache kuwafuatia ndugu zao?” 27 Yoabu akamwambia: “Kwa hakika kama Mungu wa kweli anavyoishi, usingesema, watu hawa wangeendelea kuwafuatia ndugu zao mpaka asubuhi.” 28 Sasa Yoabu akapiga pembe, wanaume wake wakaacha kuwafuatia Waisraeli, na vita vikakoma.

29 Kisha Abneri na watu wake wakapiga mwendo kupitia Araba+ usiku huo wote, wakavuka Yordani na kupiga mwendo kupitia katika bonde lote* na mwishowe wakafika Mahanaimu.+ 30 Baada ya Yoabu kuacha kumfuatia Abneri, akawakusanya watu wote pamoja. Watumishi 19 wa Daudi walikosekana kutia ndani Asaheli. 31 Lakini watumishi wa Daudi walikuwa wamewashinda Wabenjamini na wanaume wa Abneri, na wanaume 360 kati yao walikuwa wameuawa. 32 Wakamchukua Asaheli+ na kumzika katika kaburi la baba yake huko Bethlehemu.+ Kisha Yoabu na wanaume wake wakapiga mwendo usiku kucha, wakafika Hebroni+ wakati wa mapambazuko.

3 Vita kati ya nyumba ya Sauli na nyumba ya Daudi viliendelea kwa muda mrefu; Daudi akazidi kupata nguvu,+ lakini nyumba ya Sauli ikazidi kudhoofika hatua kwa hatua.+

2 Wakati huo, Daudi akazaa wana huko Hebroni.+ Mzaliwa wake wa kwanza aliitwa Amnoni+ na mama yake alikuwa Ahinoamu+ wa Yezreeli. 3 Mzaliwa wake wa pili alikuwa Kileabu na mama yake alikuwa Abigaili,+ mjane wa Nabali Mkarmeli; na wa tatu alikuwa Absalomu+ mwana wa Maaka, binti ya Talmai+ mfalme wa Geshuri. 4 Wa nne alikuwa Adoniya+ mwana wa Hagithi, na wa tano alikuwa Shefatia mwana wa Abitali. 5 Wa sita alikuwa Ithreamu mwana wa Egla, mke wa Daudi. Hao ndio wana ambao Daudi aliwazaa huko Hebroni.

6 Vita kati ya nyumba ya Sauli na nyumba ya Daudi vilipokuwa vikiendelea, Abneri+ aliendelea kuimarisha cheo chake katika nyumba ya Sauli. 7 Awali Sauli alikuwa na suria aliyeitwa Rispa,+ binti ya Aya. Baadaye Ish-boshethi+ akamuuliza Abneri: “Kwa nini ulifanya ngono na suria wa baba yangu?”+ 8 Abneri akakasirika sana kwa sababu ya maneno ya Ish-boshethi na kusema: “Je, mimi ni kichwa cha mbwa kutoka Yuda? Mpaka leo, nimeitendea kwa upendo mshikamanifu nyumba ya Sauli baba yako, ndugu zake, na rafiki zake, nami sijakusaliti kwa kukutia mikononi mwa Daudi; lakini leo unanishutumu kwa sababu ya kosa linalohusu mwanamke. 9 Mungu na aniadhibu mimi Abneri, tena vikali, nisipomtendea Daudi kama Yehova alivyomwapia:+ 10 kwamba atauhamisha ufalme kutoka katika nyumba ya Sauli na kuimarisha kiti cha ufalme cha Daudi juu ya Israeli na juu ya Yuda, kuanzia Dani mpaka Beer-sheba.”+ 11 Ish-boshethi hakuthubutu kumwambia Abneri hata neno moja zaidi, kwa sababu alimwogopa Abneri.+

12 Papo hapo Abneri akawatuma wajumbe kwa Daudi, akisema: “Nchi hii ni ya nani?” Akaongezea: “Fanya agano pamoja nami, nami nitafanya lolote niwezalo* kuwageuza Waisraeli wote wawe upande wako.”+ 13 Daudi akamwambia: “Vema! Nitafanya agano pamoja nawe. Lakini nakuomba ufanye jambo moja tu, usithubutu kuja mbele yangu mpaka umlete kwanza Mikali,+ binti ya Sauli, utakapokuja kuniona.” 14 Kisha Daudi akawatuma wajumbe kwa Ish-boshethi,+ mwana wa Sauli, akisema: “Nipe mke wangu Mikali, niliyemchumbia kwa magovi 100 ya Wafilisti.”+ 15 Kwa hiyo Ish-boshethi akawatuma watu wamchukue Mikali kutoka kwa Paltieli+ mumewe, mwana wa Laishi. 16 Lakini mume wake akaenda pamoja naye, akamfuata akilia mpaka Bahurimu.+ Kisha Abneri akamwambia: “Nenda zako, rudi!” Kwa hiyo akarudi.

17 Basi Abneri akatuma ujumbe kwa wazee wa Israeli, akisema: “Kwa muda fulani mlitaka Daudi awe mfalme wenu. 18 Sasa chukueni hatua, kwa maana Yehova alimwambia hivi Daudi: ‘Kwa mkono wako wewe Daudi mtumishi wangu+ nitawaokoa watu wangu Waisraeli kutoka mikononi mwa Wafilisti na kutoka mikononi mwa maadui wao wote.’” 19 Ndipo Abneri akazungumza na watu wa Benjamini.+ Pia, Abneri akaenda kuzungumza na Daudi faraghani kule Hebroni ili kumwambia mambo ambayo Waisraeli na nyumba yote ya Benjamini walikuwa wamekubaliana.

20 Abneri alipofika kwa Daudi kule Hebroni akiwa na wanaume 20, Daudi alimwandalia karamu pamoja na wanaume waliokuwa naye. 21 Halafu Abneri akamwambia Daudi: “Acha niende nikawakusanye pamoja Waisraeli wote kwako bwana wangu mfalme, ili wafanye agano pamoja nawe, nawe utakuwa mfalme juu ya kila kitu upendacho.”* Basi Daudi akamruhusu Abneri aende, akaenda zake kwa amani.

22 Wakati huohuo, watumishi wa Daudi na pia Yoabu walirudi baada ya kufanya uvamizi, walileta nyara nyingi sana. Abneri hakuwa tena pamoja na Daudi huko Hebroni, kwa maana alikuwa amemruhusu aende zake kwa amani. 23 Yoabu+ alipowasili na jeshi lote lililokuwa pamoja naye, aliambiwa hivi: “Abneri+ mwana wa Neri+ alikuja kwa mfalme, naye akamruhusu aende zake, na Abneri akaenda zake kwa amani.” 24 Basi Yoabu akaingia kwa mfalme na kumwambia: “Umefanya nini? Abneri alikuja kwako. Kwa nini ulimruhusu aende zake, akafanikiwa kutoroka? 25 Unamjua Abneri mwana wa Neri! Alikuja hapa kukupumbaza, kuchunguza shughuli zako zote, na kujua kila jambo unalofanya.”

26 Basi Yoabu akaondoka mbele ya Daudi, akawatuma wajumbe wamfuatie Abneri, wakamkuta kwenye tangi la maji la Sira na kumrudisha; lakini Daudi hakujua lolote kuhusu jambo hilo. 27 Abneri aliporudi Hebroni,+ Yoabu akampeleka pembeni ndani ya lango ili azungumze naye faraghani. Hata hivyo, Yoabu akamchoma kwa upanga tumboni, naye akafa;+ kwa sababu alimuua* Asaheli ndugu yake.+ 28 Daudi aliposikia habari hizo baadaye, alisema: “Mimi na ufalme wangu hatuna hatia milele mbele za Yehova kwa sababu ya damu+ ya Abneri mwana wa Neri. 29 Na irudi juu ya kichwa cha Yoabu+ na juu ya nyumba yote ya baba yake. Nyumba ya Yoabu isikose kamwe mwanamume anayetokwa na umajimaji+ au mtu mwenye ukoma+ au mwanamume anayetumikia kwenye gurudumu la mfumaji* au anayeuawa kwa upanga au asiye na chakula!”+ 30 Basi Yoabu na Abishai+ ndugu yake walimuua Abneri+ kwa sababu alimuua Asaheli ndugu yao vitani+ kule Gibeoni.

31 Kisha Daudi akamwambia Yoabu na watu wote waliokuwa pamoja naye: “Rarueni mavazi yenu na mvae nguo za magunia, mwombolezeeni Abneri kwa sauti.” Mfalme Daudi mwenyewe alikuwa akitembea nyuma ya machela ya kubebea maiti. 32 Walimzika Abneri huko Hebroni; na mfalme akalia kwa sauti kubwa kwenye kaburi la Abneri, na watu wote wakalia. 33 Mfalme akamwimbia Abneri wimbo wa maombolezo akisema:

“Je, Abneri alipaswa kufa kama anavyokufa mtu mpumbavu?

34 Mikono yako haikuwa imefungwa,

Na miguu yako haikuwa imefungwa pingu.*

Ulianguka kama mtu anayeangushwa na wahalifu.”*+

Ndipo watu wote wakamlilia tena.

35 Baadaye watu wote wakaja kumpa Daudi mkate wa faraja* kungali mchana, lakini Daudi akaapa hivi: “Mungu na aniadhibu, tena vikali, ikiwa nitaonja mkate au kitu kingine chochote kabla ya jua kutua!”+ 36 Watu wote wakaona jambo hilo, nalo likawapendeza. Watu wote walipendezwa na jambo hilo kama walivyopendezwa na mambo yote yaliyofanywa na mfalme. 37 Basi watu wote* na Waisraeli wote wakajua siku hiyo kwamba si mfalme aliyeagiza Abneri mwana wa Neri auawe.+ 38 Kisha mfalme akawaambia hivi watumishi wake: “Je, hamjui kwamba mkuu na mtu mashuhuri ameanguka leo katika Israeli?+ 39 Niko dhaifu leo, ingawa nimetiwa mafuta kuwa mfalme,+ na wanaume hawa, wana wa Seruya,+ ni wakatili sana kwangu.+ Yehova na amlipe mtenda maovu kulingana na uovu wake mwenyewe.”+

4 Ish-boshethi+ mwana wa Sauli aliposikia kwamba Abneri amekufa huko Hebroni,+ alipoteza ujasiri* na Waisraeli wote wakashikwa na wasiwasi. 2 Kulikuwa na wanaume wawili waliosimamia makundi ya wavamizi ya mwana wa Sauli: mmoja wao aliitwa Baana na mwingine aliitwa Rekabu. Walikuwa wana wa Rimoni Mbeerothi, wa kabila la Benjamini. (Kwa maana awali Beerothi+ pia lilihesabiwa kuwa sehemu ya Benjamini. 3 Wabeerothi walikimbilia Gitaimu,+ nao wamekuwa wakaaji wageni katika eneo hilo mpaka leo.)

4 Sasa Yonathani+ mwana wa Sauli alikuwa na mwana aliyelemaa miguu.*+ Alikuwa na umri wa miaka mitano wakati habari kuhusu Sauli na Yonathani zilipofika kutoka Yezreeli,+ mlezi wake akambeba na kukimbia, lakini alipokuwa akikimbia kwa woga, mwana huyo alianguka na kulemaa. Mwana huyo aliitwa Mefiboshethi.+

5 Rekabu na Baana, wana wa Rimoni Mbeerothi, walienda nyumbani kwa Ish-boshethi mchana wakati wa jua kali, alipokuwa akipumzika adhuhuri. 6 Wakaingia nyumbani mwake kana kwamba wamekuja kuchukua ngano, wakampiga tumboni; kisha Rekabu na Baana+ ndugu yake wakakimbia. 7 Walipoingia nyumbani, alikuwa amelala kitandani mwake katika chumba chake cha kulala, wakampiga na kumuua, kisha wakamkata kichwa. Halafu wakakichukua na kutembea usiku kucha kwenye barabara inayoenda Araba. 8 Wakamletea Daudi kichwa cha Ish-boshethi+ huko Hebroni na kumwambia mfalme: “Ndicho hiki kichwa cha Ish-boshethi mwana wa Sauli adui yako+ aliyetaka kukuua.+ Leo hii Yehova amekulipizia kisasi bwana wangu mfalme dhidi ya Sauli na wazao wake.”

9 Hata hivyo, Daudi akamjibu hivi Rekabu na Baana ndugu yake, wana wa Rimoni Mbeerothi: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, aliyeniokoa* kutoka katika taabu zote,+ 10 mtu fulani aliponiambia, ‘Sauli amekufa,’+ akifikiri ananiletea habari njema, nilimkamata na kumuua+ kule Siklagi. Hayo ndiyo malipo ya mjumbe aliyopokea kutoka kwangu! 11 Itakuwaje wakati wanaume waovu wamemuua mtu mwadilifu nyumbani mwake mwenyewe akiwa katika kitanda chake? Kwa nini nisidai damu yake kutoka mikononi mwenu+ na kuwaangamiza kutoka duniani?” 12 Kisha Daudi akawaamuru vijana wake wawaue.+ Wakawakata mikono na miguu yao na kuwatundika+ kando ya kidimbwi kilicho Hebroni. Lakini wakachukua kichwa cha Ish-boshethi na kukizika katika kaburi la Abneri huko Hebroni.

5 Baada ya muda makabila yote ya Israeli yakaja kwa Daudi huko Hebroni+ na kusema: “Tazama! Sisi ni mfupa wako na nyama yako.*+ 2 Zamani, Sauli alipokuwa mfalme wetu, ni wewe uliyewaongoza Waisraeli vitani.*+ Na Yehova alikuambia hivi: ‘Utawachunga watu wangu Waisraeli, nawe utakuwa kiongozi wa Israeli.’”+ 3 Basi wazee wote wa Israeli wakaja kwa mfalme huko Hebroni, na Mfalme Daudi akafanya agano nao+ huko Hebroni mbele za Yehova. Kisha wakamtia mafuta Daudi awe mfalme wa Israeli.+

4 Daudi alikuwa na umri wa miaka 30 alipowekwa kuwa mfalme, naye alitawala kwa miaka 40.+ 5 Huko Hebroni alitawala Yuda kwa miaka 7 na miezi 6, na huko Yerusalemu+ alitawala Israeli yote na Yuda kwa miaka 33. 6 Mfalme na wanaume wake wakaenda Yerusalemu kuwashambulia Wayebusi+ waliokuwa wakiishi nchini. Walimdhihaki Daudi wakisema: “Hutaingia humu kamwe! Hata vipofu na vilema watakufukuza.” Hivi ndivyo walivyofikiri: ‘Daudi hataingia humu kamwe.’+ 7 Hata hivyo, Daudi akaiteka ngome ya Sayuni, ambayo sasa ni Jiji la Daudi.+ 8 Basi siku hiyo Daudi akasema: “Wale wanaowashambulia Wayebusi wanapaswa kupitia kwenye mfereji wa maji ili wawaue ‘vilema na vipofu,’ wanaomchukia Daudi!”* Ndiyo sababu watu wanasema: “Vipofu na vilema hawataingia nyumbani.” 9 Kisha Daudi akaanza kukaa katika ngome hiyo, nayo ikaitwa* Jiji la Daudi; na Daudi akaanza kujenga pande zote kuanzia kwenye Kilima*+ kuja ndani.+ 10 Kwa hiyo Daudi akawa mkuu zaidi na zaidi,+ na Yehova Mungu wa majeshi alikuwa pamoja naye.+

11 Mfalme Hiramu+ wa Tiro akawatuma wajumbe kwa Daudi, na kupeleka mbao za mierezi,+ maseremala, na waashi wa kujenga kuta, nao wakaanza kumjengea Daudi nyumba.*+ 12 Na Daudi akajua kwamba Yehova alikuwa amemwimarisha kabisa kuwa mfalme wa Israeli+ na kwamba alikuwa ameukweza ufalme wake+ kwa ajili ya watu Wake Waisraeli.+

13 Baada ya kutoka Hebroni, Daudi alichukua masuria+ na wake zaidi huko Yerusalemu, nao wakamzalia Daudi wana na mabinti zaidi.+ 14 Haya ndiyo majina ya watoto wake waliozaliwa Yerusalemu: Shamua, Shobabu, Nathani,+ Sulemani,+ 15 Ibhari, Elishua, Nefegi, Yafia, 16 Elishama, Eliada, na Elifeleti.

17 Wafilisti waliposikia kwamba Daudi alikuwa ametiwa mafuta kuwa mfalme wa Waisraeli wote,+ Wafilisti wote wakapanda kuja kumtafuta Daudi.+ Daudi aliposikia jambo hilo, akashuka kuingia ndani ya ngome.+ 18 Kisha Wafilisti wakaja na kuenea katika Bonde la* Refaimu.+ 19 Daudi akamuuliza Yehova:+ “Je, nipande kwenda kuwashambulia Wafilisti? Je, utawatia mikononi mwangu?” Ndipo Yehova akamwambia Daudi: “Panda uende, nami hakika nitawatia Wafilisti mikononi mwako.”+ 20 Basi Daudi akaenda Baal-perasimu na kuwaua huko. Ndipo akasema: “Yehova amewapasua na kuwapita+ maadui wangu mbele yangu, kama ufa uliopasuliwa na maji.” Ndiyo sababu alipaita mahali hapo Baal-perasimu.*+ 21 Wafilisti wakaacha sanamu zao hapo, na Daudi na wanaume wake wakazichukua na kwenda nazo.

22 Baadaye Wafilisti wakaja tena na kuenea katika Bonde la* Refaimu.+ 23 Daudi akamwomba Yehova ushauri, lakini Akasema: “Usipande moja kwa moja. Badala yake, zunguka nyuma yao, uwashambulie mbele ya vichaka vya mibaka. 24 Na utakaposikia sauti ya watu wakipiga mwendo juu ya vichaka vya mibaka, tenda bila kusita, kwa sababu mimi Yehova nitakuwa nimetangulia mbele yako kuliua jeshi la Wafilisti.” 25 Basi Daudi akafanya kama Yehova alivyomwamuru, akawaua Wafilisti+ kuanzia Geba+ mpaka Gezeri.+

6 Daudi akawakusanya tena wanajeshi wote walio bora wa Israeli, wanaume 30,000. 2 Kisha Daudi na wanaume wote waliokuwa pamoja naye wakaondoka kwenda Baale-yuda ili kuleta Sanduku la Mungu wa kweli+ kutoka huko, ambalo mbele yake watu hulisifu jina la Yehova wa majeshi,+ anayeketi kwenye kiti cha ufalme juu ya* makerubi.+ 3 Hata hivyo, wakaweka Sanduku la Mungu wa kweli juu ya gari jipya la kukokotwa+ ili walisafirishe kutoka katika nyumba ya Abinadabu,+ iliyokuwa kwenye kilima; na Uza na Ahio, wana wa Abinadabu, walikuwa wakiliongoza gari hilo jipya.

4 Basi wakalisafirisha Sanduku la Mungu wa kweli kutoka katika nyumba ya Abinadabu iliyokuwa kwenye kilima, na Ahio alikuwa akitembea mbele ya Sanduku hilo. 5 Daudi na nyumba yote ya Israeli walikuwa wakisherehekea mbele za Yehova kwa ala za kila aina zilizotengenezwa kwa mbao za mberoshi, vinubi, vinanda vinginevyo,+ matari,+ matasa, na matoazi.+ 6 Lakini walipofika kwenye uwanja wa kupuria wa Nakoni, Uza akaunyoosha mkono wake haraka na kulikamata Sanduku la Mungu wa kweli,+ kwa sababu ng’ombe walikuwa karibu kuliangusha. 7 Ndipo hasira ya Yehova ikawaka dhidi ya Uza, na Mungu wa kweli akamuua+ papo hapo kwa sababu ya tendo lake lisilo la heshima,+ akafa hapo karibu na Sanduku la Mungu wa kweli. 8 Lakini Daudi akakasirika kwa sababu hasira kali ya Yehova iliwaka dhidi ya Uza; na tangu siku hiyo mahali hapo panaitwa Peres-uza.* 9 Basi Daudi akamwogopa Yehova+ siku hiyo na kusema: “Sanduku la Yehova linawezaje kuja kwangu?”+ 10 Daudi hakutaka kuleta Sanduku la Yehova mahali alipokuwa katika Jiji la Daudi.+ Badala yake, Daudi aliagiza lipelekwe katika nyumba ya Obed-edomu,+ Mgathi.

11 Sanduku la Yehova likaendelea kukaa katika nyumba ya Obed-edomu Mgathi kwa miezi mitatu, na Yehova akazidi kumbariki Obed-edomu na nyumba yake yote.+ 12 Mfalme Daudi akaambiwa hivi: “Yehova ameibariki nyumba ya Obed-edomu na vitu vyake vyote kwa sababu ya Sanduku la Mungu wa kweli.” Basi Daudi akaenda kulichukua Sanduku la Mungu wa kweli kutoka katika nyumba ya Obed-edomu na kulipandisha kwa shangwe katika Jiji la Daudi.+ 13 Wale waliobeba+ Sanduku la Yehova walipokuwa wamepiga hatua sita, Daudi alitoa dhabihu ya ng’ombe dume na mnyama aliyenoneshwa.

14 Daudi alikuwa akicheza dansi huku na huku mbele za Yehova kwa nguvu zake zote; na wakati wote huo Daudi alikuwa amevaa* efodi ya kitani.+ 15 Daudi na nyumba yote ya Israeli walikuwa wakilipandisha Sanduku+ la Yehova kwa kelele za shangwe+ na sauti ya pembe.+ 16 Lakini Sanduku la Yehova lilipoingia katika Jiji la Daudi, Mikali,+ binti ya Sauli, akaangalia chini kupitia dirishani, akamwona Mfalme Daudi akirukaruka na kucheza dansi huku na huku mbele za Yehova; naye akaanza kumdharau moyoni mwake.+ 17 Basi wakaliingiza ndani Sanduku la Yehova na kuliweka mahali pake ndani ya hema ambalo Daudi alikuwa amepiga ili aliweke humo.+ Kisha Daudi akatoa dhabihu za kuteketezwa+ na dhabihu za ushirika+ mbele za Yehova.+ 18 Daudi alipomaliza kutoa dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ushirika, akawabariki watu katika jina la Yehova wa majeshi.⁠ 19 Pia, akawagawia watu wote, umati wote wa Waisraeli, kila mwanamume na mwanamke mkate wa mviringo, keki ya tende, na keki ya zabibu kavu, halafu watu wote wakaenda zao, kila mmoja nyumbani kwake mwenyewe.

20 Daudi aliporudi ili kuwabariki watu wa nyumba yake mwenyewe, Mikali, binti ya Sauli+ akatoka nje kumpokea Daudi. Mikali akasema: “Mfalme wa Israeli amejitukuza kwelikweli leo kwa kujifunua leo mbele ya macho ya vijakazi wa watumishi wake, kama tu mtu asiye na akili anavyojifunua waziwazi!”+ 21 Ndipo Daudi akamwambia Mikali: “Nilikuwa nikisherehekea mbele za Yehova, aliyenichagua mimi badala ya baba yako na nyumba yake yote na ambaye aliniweka mimi kuwa kiongozi wa watu wa Yehova, Waisraeli.+ Kwa hiyo, nitasherehekea mbele za Yehova, 22 nami nitajinyenyekeza zaidi hata kuliko nilivyofanya na kuwa mdogo hata machoni pangu mwenyewe. Lakini nitatukuzwa na hao vijakazi uliowataja.” 23 Basi Mikali,+ binti ya Sauli, hakuwa na watoto mpaka siku alipokufa.

7 Mfalme alipoanza kuishi katika nyumba yake mwenyewe*+ na baada ya Yehova kumpumzisha kutokana na maadui wake wote waliomzunguka, 2 mfalme alimwambia hivi nabii Nathani:+ “Mimi hapa ninaishi katika nyumba ya mierezi+ huku Sanduku la Mungu wa kweli likikaa katikati ya vitambaa vya mahema.”+ 3 Nathani akamwambia mfalme: “Nenda ufanye jambo lolote lililo moyoni mwako, kwa sababu Yehova yuko pamoja nawe.”+

4 Usiku huohuo, neno hili la Yehova likamjia Nathani: 5 “Nenda ukamwambie mtumishi wangu Daudi, ‘Yehova anasema hivi: “Je, utanijengea nyumba nikae ndani yake?+ 6 Kwa maana sijakaa ndani ya nyumba tangu siku nilipowatoa watu wa Israeli huko Misri mpaka leo,+ bali nimekuwa nikihama* huku na kule katika hema na katika hema la ibada.+ 7 Wakati wote nilipotembea na Waisraeli wote,* je, niliwahi wakati wowote kumuuliza kiongozi yeyote wa kabila la Israeli niliyemweka awachunge watu wangu Waisraeli, ‘Kwa nini hukunijengea nyumba ya mierezi?’”’ 8 Sasa mwambie hivi mtumishi wangu Daudi: ‘Yehova wa majeshi anasema hivi: “Nilikutoa malishoni, ili usiendelee kuchunga kondoo,+ uwe kiongozi wa watu wangu Waisraeli.+ 9 Nami nitakuwa pamoja nawe popote utakapoenda,+ nami nitawaangamiza maadui wako wote kutoka mbele yako;+ nami nitafanya jina lako liwe maarufu+ kama jina la watu maarufu duniani. 10 Nitachagua mahali kwa ajili ya watu wangu Waisraeli na kuwaweka humo, nao wataishi humo na hawatasumbuliwa tena; na watu waovu hawatawakandamiza tena kama walivyofanya zamani,+ 11 tangu siku nilipowaweka waamuzi+ juu ya watu wangu Waisraeli. Nami nitakupumzisha kutokana na maadui wako wote.+

“‘“Pia, Yehova amekuambia kwamba Yehova atakujengea nyumba.*+ 12 Siku zako zitakapokwisha+ nawe ufe na kuzikwa pamoja na mababu zako, ndipo nitakapomwinua mzao wako* baada yako, mwana wako mwenyewe,* nami nitauimarisha kabisa ufalme wake.+ 13 Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa ajili ya jina langu,+ nami nitakiimarisha kabisa kiti cha ufalme wake milele.+ 14 Nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu.+ Atakapokosea, nitamkaripia kwa fimbo ya wanadamu na kwa viboko vya wana wa binadamu.*+ 15 Upendo wangu mshikamanifu hautaondolewa kwake kama nilivyouondoa kwa Sauli,+ niliyemwondoa kutoka mbele yako. 16 Nyumba yako na ufalme wako utakuwa salama milele mbele yako; kiti chako cha ufalme kitaimarishwa kabisa milele.”’”+

17 Nathani akamwambia Daudi maneno hayo yote na maono hayo yote.+

18 Ndipo Mfalme Daudi akaingia na kuketi mbele za Yehova na kusema: “Mimi ni nani, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova? Na nyumba yangu ni nini hivi kwamba umenileta mpaka hapa nilipofika?+ 19 Na kana kwamba hilo halitoshi, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, unasema pia kwamba nyumba yangu mimi mtumishi wako itadumu kwa muda mrefu; na haya ni maagizo* kwa wanadamu wote, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. 20 Mimi mtumishi wako Daudi nitakwambia nini zaidi wakati unanijua vizuri sana,+ Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova? 21 Kwa ajili ya neno lako na kupatana na moyo wako* umetenda mambo haya yote makuu na kunifunulia mimi mtumishi wako.+ 22 Ndiyo sababu wewe kwa kweli ni mkuu,+ Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. Hakuna aliye kama wewe,+ na hakuna Mungu ila wewe;+ mambo yote tuliyosikia kwa masikio yetu yanathibitisha jambo hilo. 23 Na kuna taifa gani lingine duniani lililo kama watu wako Waisraeli?+ Wewe Mungu ulienda na kuwakomboa wakiwa watu wako,+ ukajijengea jina+ kwa kufanya mambo makuu na yenye kuogopesha kwa ajili yao.+ Uliyafukuza mataifa na miungu yao kwa ajili ya watu wako, ambao uliwakomboa kutoka Misri kwa ajili yako mwenyewe. 24 Uliwaimarisha watu wako Waisraeli ili wawe watu wako milele;+ na wewe, Ee Yehova, umekuwa Mungu wao.+

25 “Sasa, Ee Yehova Mungu, timiza ahadi uliyotoa kunihusu mimi mtumishi wako na nyumba yangu milele, na ufanye kama ulivyoahidi.+ 26 Jina lako na likwezwe milele,+ ili watu waseme, ‘Yehova wa majeshi ni Mungu wa Israeli,’ na nyumba yangu mimi mtumishi wako Daudi na iimarishwe kabisa mbele zako.+ 27 Kwa maana wewe, Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, umenifunulia mimi mtumishi wako ukisema, ‘Nitakujengea nyumba.’*+ Ndiyo sababu mimi mtumishi wako nina ujasiri wa* kutoa sala hii kwako. 28 Na sasa, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, wewe ndiye Mungu wa kweli, na maneno yako ni kweli,+ nawe umeniahidi mimi mtumishi wako mambo hayo mema. 29 Basi na ufurahie kuibariki nyumba yangu mimi mtumishi wako, na idumu milele mbele zako;+ kwa sababu wewe, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, umeahidi, na kwa baraka yako, nyumba yangu mimi mtumishi wako na ibarikiwe milele.”+

8 Baadaye, Daudi aliwashinda Wafilisti+ na kuwatiisha,+ akachukua jiji la Metheg-ama kutoka mikononi mwa Wafilisti.

2 Akawashinda Wamoabu+ na kuwaamuru walale chini ardhini, naye akawapima kwa kamba. Alipima safu mbili za watu ambao wangeuawa, na safu moja nzima ya watu ambao hawangeuawa.+ Wamoabu wakawa watumishi wa Daudi na kumletea ushuru.+

3 Daudi alimshinda Hadadezeri mwana wa Rehobu mfalme wa Soba+ mfalme huyo alipokuwa akienda kurudisha mamlaka yake katika eneo la Mto Efrati.+ 4 Daudi akawateka wapanda farasi 1,700 na wanajeshi wake 20,000 wanaotembea kwa miguu. Kisha Daudi akawakata farasi wote mishipa ya miguu isipokuwa farasi 100 waliokokota magari.+

5 Wasiria wa Damasko+ walipokuja kumsaidia Mfalme Hadadezeri wa Soba, Daudi aliwaua Wasiria 22,000.+ 6 Halafu Daudi akaweka kambi za kijeshi kule Siria ya Damasko, na Wasiria wakawa watumishi wa Daudi na kumletea ushuru. Yehova alimpa Daudi ushindi* popote alipoenda.+ 7 Isitoshe, Daudi alichukua ngao za mviringo za dhahabu kutoka kwa watumishi wa Hadadezeri na kuzileta Yerusalemu.+ 8 Mfalme Daudi alichukua shaba nyingi sana kutoka Beta na Berothai, majiji ya Hadadezeri.

9 Basi Mfalme Toi wa Hamathi+ akasikia kwamba Daudi alikuwa amelishinda jeshi lote la Hadadezeri.+ 10 Kwa hiyo Toi akamtuma Yoramu mwana wake kwa Mfalme Daudi ili amjulie hali na kumpongeza kwa sababu alikuwa amepigana na Hadadezeri na kumshinda (kwa maana mara nyingi Hadadezeri alimshambulia Toi); na Yoramu alimletea Daudi vitu vya fedha, dhahabu, na shaba. 11 Mfalme Daudi akavitakasa vitu hivyo ili viwe vya Yehova, pamoja na fedha na dhahabu aliyotakasa kutoka kwa mataifa yote aliyokuwa ameyashinda:+ 12 kutoka Siria na kutoka Moabu,+ kutoka kwa Waamoni, Wafilisti,+ Waamaleki,+ na kutoka katika nyara za Hadadezeri+ mwana wa Rehobu mfalme wa Soba. 13 Pia Daudi alijijengea jina aliporudi baada ya kuwaua Waedomu 18,000 katika Bonde la Chumvi.+ 14 Aliweka kambi za kijeshi huko Edomu. Aliweka kambi za kijeshi katika nchi yote ya Edomu, na Waedomu wote wakawa watumishi wa Daudi.+ Yehova alimpa Daudi ushindi* popote alipoenda.+

15 Daudi akaendelea kutawala Israeli yote,+ naye aliwatawala watu wake wote+ kwa haki na uadilifu.+ 16 Yoabu+ mwana wa Seruya alikuwa mkuu wa jeshi, na Yehoshafati+ mwana wa Ahiludi alifanya kazi ya kuweka kumbukumbu. 17 Sadoki+ mwana wa Ahitubu na Ahimeleki mwana wa Abiathari walikuwa makuhani, na Seraya alikuwa mwandishi. 18 Benaya+ mwana wa Yehoyada aliwasimamia Wakerethi na Wapelethi.+ Na wana wa Daudi walikuwa wahudumu wakuu.*

9 Kisha Daudi akauliza: “Je, kuna yeyote aliyebaki katika nyumba ya Sauli ninayeweza kumtendea kwa upendo mshikamanifu kwa ajili ya Yonathani?”+ 2 Basi kulikuwa na mtumishi wa nyumba ya Sauli aliyeitwa Siba.+ Kwa hiyo wakamwita aje kwa Daudi, na mfalme akamuuliza: “Je, wewe ni Siba?” Akajibu: “Ni mimi mtumishi wako.” 3 Mfalme akaendelea kumuuliza: “Je, kuna yeyote aliyebaki katika nyumba ya Sauli ninayeweza kumtendea kwa upendo mshikamanifu wa Mungu?” Siba akamjibu hivi mfalme: “Bado kuna mwana mmoja wa Yonathani; amelemaa miguu yote miwili.”*+ 4 Mfalme akamuuliza: “Yuko wapi?” Siba akamjibu mfalme: “Yuko katika nyumba ya Makiri+ mwana wa Amieli kule Lo-debari.”

5 Mara moja Mfalme Daudi akaagiza aletwe kutoka katika nyumba ya Makiri mwana wa Amieli kule Lo-debari. 6 Mefiboshethi mwana wa Yonathani mwana wa Sauli alipofika mbele ya Daudi, mara moja alianguka chini kifudifudi na kumwinamia. Daudi akasema: “Mefiboshethi!” naye akajibu: “Mimi hapa, mtumishi wako.” 7 Daudi akamwambia: “Usiogope, kwa maana hakika nitakutendea kwa upendo mshikamanifu+ kwa ajili ya Yonathani baba yako, nami nitakurudishia ardhi yote ya Sauli babu yako, nawe utakula chakula* mezani pangu sikuzote.”+

8 Basi akainama na kusema: “Mimi mtumishi wako ni nani, hivi kwamba umenitendea kwa fadhili* mbwa mfu+ kama mimi?” 9 Sasa mfalme akaagiza Siba mtumishi wa Sauli aitwe, akamwambia: “Kila kitu ambacho kilikuwa cha Sauli na nyumba yake yote ninampa mjukuu wa bwana wako.+ 10 Wewe na wana wako na watumishi wako mtamlimia shamba lake, nanyi mtayakusanya mavuno ya shamba hilo ili watu wa nyumbani mwa mjukuu wa bwana wako wapate chakula. Lakini Mefiboshethi, mjukuu wa bwana wako, atakula chakula mezani pangu sikuzote.”+

Siba alikuwa na wana 15 na watumishi 20.+ 11 Ndipo Siba akamwambia mfalme: “Mimi mtumishi wako nitafanya mambo yote ambayo bwana wangu mfalme unaniamuru mimi mtumishi wako nifanye.” Basi Mefiboshethi akawa akila kwenye meza ya Daudi* kama mmoja wa wana wa mfalme. 12 Sasa Mefiboshethi pia alikuwa na mtoto mdogo wa kiume aliyeitwa Mika;+ na watu wote walioishi katika nyumba ya Siba wakawa watumishi wa Mefiboshethi. 13 Naye Mefiboshethi aliishi Yerusalemu kwa maana sikuzote alikula mezani pa mfalme;+ na miguu yake ilikuwa imelemaa.+

10 Baadaye mfalme wa Waamoni+ akafa, na Hanuni mwanawe akawa mfalme baada yake.+ 2 Ndipo Daudi akasema: “Nitamtendea kwa upendo mshikamanifu Hanuni mwana wa Nahashi kama baba yake alivyonitendea kwa upendo mshikamanifu.” Basi Daudi akawatuma watumishi wake ili wamfariji baada ya kufiwa na baba yake. Lakini watumishi wa Daudi walipofika katika nchi ya Waamoni, 3 wakuu wa Waamoni wakamwambia Hanuni bwana wao: “Je, unafikiri kwamba Daudi anawatuma wafariji kwako ili kumheshimu baba yako? Je, Daudi hajawatuma watumishi wake ili kulichunguza jiji lote na kulipeleleza na kuliteka?” 4 Kwa hiyo Hanuni akawachukua watumishi wa Daudi, akawanyoa nusu ya ndevu zao,+ akakata nguo zao katikati kwenye matako na kuwafukuza. 5 Daudi alipoambiwa habari hiyo, mara moja akawatuma wanaume fulani waende kukutana nao, kwa sababu watumishi hao walikuwa wameaibishwa sana; mfalme akawaambia: “Kaeni Yeriko+ mpaka ndevu zenu zitakapoota, kisha mrudi.”

6 Baada ya muda Waamoni wakaona kuwa wananuka mbele ya Daudi, kwa hiyo wakawatuma wajumbe waende kuwakodi Wasiria wa Beth-rehobu + na Wasiria wa Soba,+ wanajeshi 20,000 wanaotembea kwa miguu; na mfalme wa Maaka+ akiwa na wanaume 1,000; na kutoka Ishtobu,* wanaume 12,000.+ 7 Daudi aliposikia habari hizo, akamtuma Yoabu na jeshi lote, kutia ndani mashujaa wake hodari zaidi.+ 8 Nao Waamoni wakatoka na kujipanga kivita kwenye lango la jiji huku Wasiria wa Soba na wa Rehobu, pamoja na Ishtobu* na Maaka, wakiwa peke yao uwanjani.

9 Yoabu alipoona kwamba anashambuliwa upande wa mbele na wa nyuma, akachagua baadhi ya wanajeshi bora katika Israeli na kuwapanga kivita ili wapigane na Wasiria.+ 10 Wanaume waliobaki aliwaweka chini ya usimamizi wa* Abishai ndugu yake,+ ili awapange kivita kupigana na Waamoni.+ 11 Kisha akasema: “Ikiwa Wasiria watanizidi nguvu, basi mtaniokoa; lakini Waamoni wakiwazidi ninyi nguvu, nitawaokoa. 12 Ni lazima tuwe imara na jasiri+ kwa ajili ya watu wetu na kwa ajili ya majiji ya Mungu wetu, naye Yehova atafanya yaliyo mema machoni pake.”+

13 Kisha Yoabu na wanaume wake wakasonga mbele kwenda kupigana vita na Wasiria, nao wakamkimbia.+ 14 Waamoni walipoona kwamba Wasiria wamekimbia, wakamkimbia Abishai na kuingia jijini. Baada ya Yoabu kupigana na Waamoni akarudi Yerusalemu.

15 Wasiria walipoona kwamba wameshindwa na Waisraeli, wakajikusanya tena.+ 16 Basi Hadadezeri+ akaagiza Wasiria kutoka katika eneo la Mto Efrati+ waletwe, nao wakaja Helamu, wakiongozwa na Shobaki mkuu wa jeshi la Hadadezeri.

17 Daudi alipoambiwa habari hiyo, akawakusanya mara moja Waisraeli wote, wakavuka Yordani na kufika Helamu. Kisha Wasiria wakajipanga kivita ili kwenda kupigana na Daudi.+ 18 Lakini Wasiria wakawakimbia Waisraeli; na Daudi akawaua Wasiria 700 wanaoendesha magari ya vita na wapanda farasi 40,000, naye akampiga Shobaki mkuu wa jeshi, akafa huko.+ 19 Wafalme wote waliokuwa watumishi wa Hadadezeri walipoona kwamba wameshindwa na Waisraeli, mara moja wakafanya amani na Waisraeli, wakawa watumishi wao;+ na Wasiria wakaogopa kuwasaidia tena Waamoni.

11 Mwanzoni mwa mwaka,* wakati ambapo wafalme huenda vitani, Daudi akamtuma Yoabu na watumishi wake pamoja na jeshi lote la Israeli kuwaangamiza Waamoni, nao wakalizingira Raba,+ lakini Daudi alibaki Yerusalemu.+

2 Jioni moja Daudi aliamka kitandani akaenda kutembeatembea juu ya paa la nyumba ya mfalme.* Akiwa kwenye paa alimwona mwanamke akioga, na mwanamke huyo alikuwa mrembo sana. 3 Daudi akamtuma mtu fulani aulize kuhusu mwanamke huyo, mtu huyo akamwambia: “Ni Bath-sheba,+ binti ya Eliamu;+ mke wa Uria+ Mhiti.”+ 4 Kisha Daudi akawatuma wajumbe wamlete.+ Basi akaja kwa Daudi, naye Daudi akalala naye.+ (Wakati huo mwanamke huyo alikuwa akijitakasa uchafu wake.*)+ Kisha, mwanamke huyo akarudi nyumbani kwake.

5 Mwanamke huyo akapata mimba, akatuma ujumbe huu kwa Daudi: “Nina mimba.” 6 Ndipo Daudi akatuma ujumbe huu kwa Yoabu: “Mtume kwangu Uria Mhiti.” Basi Yoabu akamtuma Uria kwa Daudi. 7 Uria alipofika, Daudi akamuuliza habari za Yoabu, habari kuhusu wanajeshi, na kuhusu vita. 8 Kisha Daudi akamwambia Uria: “Shuka uende nyumbani kwako ukapumzike.”* Uria alipotoka nyumbani mwa mfalme, alipelekewa zawadi ya hisani kutoka kwa mfalme.* 9 Lakini Uria alilala kwenye mlango wa nyumba ya mfalme pamoja na watumishi wengine wote wa bwana wake, naye hakushuka kwenda nyumbani kwake. 10 Kwa hiyo Daudi akaambiwa: “Uria hakushuka kwenda nyumbani kwake.” Ndipo Daudi akamuuliza Uria: “Umetoka safarini, sivyo? Kwa nini hukushuka kwenda nyumbani kwako?” 11 Uria akamjibu Daudi: “Sanduku la agano+ na wanaume wa Israeli na Yuda wanakaa katika vibanda, na bwana wangu Yoabu na watumishi wake wanapiga kambi uwanjani. Ninawezaje kwenda nyumbani kwangu kula na kunywa na kulala na mke wangu?+ Kwa hakika kama unavyoishi na kama ulivyo hai,* sitafanya hivyo!”

12 Basi Daudi akamwambia Uria: “Kaa hapa leo pia, na kesho nitakuruhusu uende.” Kwa hiyo Uria akakaa Yerusalemu siku hiyo na siku iliyofuata. 13 Halafu Daudi akaagiza aitwe ili ale na kunywa pamoja naye, akamfanya alewe. Lakini jioni, Uria alienda kulala kitandani mwake pamoja na watumishi wa bwana wake, naye hakushuka kwenda nyumbani kwake. 14 Asubuhi Daudi akamwandikia Yoabu barua, akampa Uria aipeleke kwa Yoabu. 15 Katika barua hiyo, Daudi aliandika hivi: “Mwekeni Uria kwenye mstari wa mbele mahali ambapo vita ni vikali zaidi. Kisha mmwache na kurudi nyuma yake ili apigwe na kuuawa.”+

16 Yoabu alikuwa amelichunguza jiji kwa makini, basi alimweka Uria mahali ambapo alijua kuna wanajeshi mashujaa. 17 Wanaume wa jiji walipotoka nje na kupigana na Yoabu, baadhi ya watumishi wa Daudi waliuawa, na Uria Mhiti alikuwa miongoni mwa watu waliouawa.+ 18 Sasa Yoabu akampelekea Daudi habari zote za vita. 19 Alimpa mjumbe maagizo haya: “Utakapomaliza kumwambia mfalme habari zote za vita, 20 huenda mfalme atakasirika na kukuuliza, ‘Kwa nini mlienda karibu sana na jiji kupigana? Je, hamkujua kwamba watawapiga mishale kutoka juu ya ukuta? 21 Ni nani aliyemuua Abimeleki+ mwana wa Yerubeshethi?+ Je, si mwanamke aliyemwangushia jiwe la juu la kusagia kutoka juu ya ukuta na kumuua kule Thebesi? Kwa nini mlienda karibu sana na ukuta?’ Kisha utamwambia, ‘Pia mtumishi wako Uria Mhiti amekufa.’”

22 Basi mjumbe huyo akaenda na kumwambia Daudi kila jambo ambalo Yoabu alimtuma amwambie. 23 Mjumbe huyo akamwambia Daudi: “Wanaume wao walituzidi nguvu, nao walitoka ili kutushambulia uwanjani; lakini tuliwarudisha nyuma mpaka kwenye lango la jiji. 24 Na wapiga mishale walikuwa wakiwapiga kwa mishale watumishi wako kutoka juu ya ukuta, na baadhi ya watumishi wako mfalme wakafa; mtumishi wako Uria Mhiti akafa pia.”+ 25 Ndipo Daudi akamwambia mjumbe huyo: “Mwambie hivi Yoabu: ‘Jambo hili lisikuhangaishe, kwa maana upanga humnyafua huyu na pia yule. Zidisheni mashambulizi dhidi ya jiji na mlishinde.’+ Nawe umtie moyo.”

26 Mke wa Uria aliposikia kwamba Uria mume wake amekufa, akaanza kumwombolezea mume wake. 27 Mara tu kipindi cha kuomboleza kilipokwisha, Daudi akaagiza aletwe nyumbani kwake, akawa mke wake+ na kumzalia mwana. Lakini jambo ambalo Daudi alikuwa amefanya lilimchukiza sana* Yehova.+

12 Kwa hiyo Yehova akamtuma Nathani+ kwa Daudi. Akafika kwake+ na kumwambia: “Kulikuwa na wanaume wawili katika jiji moja, mmoja alikuwa tajiri na mwingine maskini. 2 Yule mwanamume tajiri alikuwa na kondoo wengi sana na ng’ombe;+ 3 lakini yule mwanamume maskini hakuwa na chochote isipokuwa mwanakondoo mmoja jike mdogo aliyekuwa amemnunua.+ Alimtunza mwanakondoo huyo, naye akakua nyumbani mwake pamoja na wanawe. Mwanakondoo huyo alikuwa akila chakula kidogo alichokuwa nacho mtu huyo na kunywea kikombe chake, naye alikuwa akilala mikononi mwake. Mwanakondoo huyo akawa kama binti kwake. 4 Baadaye mgeni alimtembelea yule mwanamume tajiri, lakini mwanamume huyo hakutaka kuchukua mmoja wa kondoo wake mwenyewe au ng’ombe wake ili amchinjie msafiri aliyemtembelea. Badala yake alimchukua mwanakondoo wa yule mwanamume maskini na kumchinjia mgeni aliyemtembelea.”+

5 Daudi aliposikia hayo, alikasirika sana kwa sababu ya mwanamume huyo, akamwambia Nathani: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi,+ mwanamume aliyefanya hivyo anastahili kufa! 6 Naye anapaswa kulipa mara nne zaidi kwa ajili ya mwanakondoo huyo,+ kwa sababu alifanya jambo hilo na hakuwa na huruma.”

7 Ndipo Nathani akamwambia Daudi: “Mwanamume huyo ni wewe! Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Mimi mwenyewe nilikutia mafuta uwe mfalme wa Israeli,+ nami nilikuokoa kutoka mikononi mwa Sauli.+ 8 Nilikuwa tayari kukupa nyumba ya bwana wako+ na kuwaweka mikononi mwako wake za+ bwana wako, nami nikakupa nyumba ya Israeli na ya Yuda.+ Na kana kwamba hayo hayatoshi, nilikuwa tayari kukufanyia mengi zaidi.+ 9 Kwa nini ulilidharau neno la Yehova, kwa kutenda lililo ovu machoni pake? Ulimuua Uria Mhiti kwa upanga!+ Kisha ukamchukua mke wake awe mke wako+ baada ya kumuua Uria kwa upanga wa Waamoni.+ 10 Sasa upanga hautaondoka nyumbani mwako,+ kwa sababu ulinidharau kwa kumchukua mke wa Uria Mhiti awe mke wako.’ 11 Yehova anasema hivi: ‘Tazama, ninakuletea msiba kutoka katika nyumba yako mwenyewe;+ na mbele ya macho yako mwenyewe, nami nitawachukua wake zako na kumpa mwanamume mwingine,+ naye atalala na wake zako kweupe kabisa wakati wa mchana.*+ 12 Ingawa ulifanya jambo hilo kwa siri,+ mimi nitafanya jambo hili mbele ya Waisraeli wote kweupe kabisa wakati wa mchana.’”*

13 Ndipo Daudi akamwambia Nathani: “Nimemtendea Yehova dhambi.”+ Nathani akamwambia Daudi: “Yehova naye amekusamehe dhambi uliyotenda.*+ Hutakufa.+ 14 Hata hivyo, kwa sababu hukumheshimu Yehova kamwe katika jambo hili, mwana wako aliyezaliwa hivi punde, hakika atakufa.”

15 Kisha Nathani akaenda nyumbani kwake.

Basi Yehova akamletea pigo mtoto ambaye mke wa Uria alikuwa amemzalia Daudi, akawa mgonjwa. 16 Daudi akamsihi sana Mungu wa kweli kwa ajili ya mvulana huyo. Daudi akafunga kabisa, naye alikuwa akiingia chumbani mwake na kulala chini usiku kucha.+ 17 Basi wazee wa nyumbani mwake wakasimama karibu naye na kujaribu kumwinua kutoka sakafuni, lakini alikataa, wala hakula pamoja nao. 18 Siku ya saba yule mtoto akafa, lakini watumishi wa Daudi wakaogopa kumwambia kwamba mtoto amekufa. Walisema: “Mtoto alipokuwa hai tulizungumza naye lakini hakutusikiliza. Sasa tutamwambiaje kwamba mtoto amekufa? Huenda akatenda jambo baya sana.”

19 Daudi alipowaona watumishi wake wakinong’onezeana, alitambua kwamba yule mtoto amekufa. Daudi akawauliza: “Mtoto amekufa?” Wakajibu: “Amekufa.” 20 Basi Daudi akainuka kutoka sakafuni. Akaoga, akajipaka mafuta,+ akabadili nguo zake, akaenda katika nyumba ya Yehova+ na kusujudu. Kisha akaenda nyumbani kwake* na kuomba aletewe chakula, naye akala. 21 Watumishi wake wakamuuliza: “Kwa nini umefanya hivi? Mtoto alipokuwa hai, ulifunga na kulia daima; lakini mara tu mtoto alipokufa ukainuka na kula chakula.” 22 Akajibu: “Mtoto alipokuwa hai, nilifunga+ na kulia daima kwa sababu nilisema moyoni, ‘Ni nani ajuaye kama Yehova atanionyesha kibali na kumwacha mtoto aishi?’+ 23 Sasa kwa kuwa amekufa, kwa nini nifunge? Je, naweza kumrudisha tena?+ Mimi nitamfuata,+ lakini yeye hatanirudia mimi.”+

24 Kisha Daudi akamfariji Bath-sheba mke wake.+ Akaingia kwake na kulala naye. Baada ya muda akazaa mwana, akapewa jina Sulemani.*+ Yehova akampenda mwana huyo,+ 25 akamtuma nabii Nathani+ amwite mtoto huyo Yedidia,* kwa ajili ya Yehova.

26 Yoabu akaendelea kupigana na jiji la Raba+ la Waamoni,+ akaliteka jiji hilo la kifalme.*+ 27 Basi Yoabu akawatuma wajumbe kwa Daudi akisema: “Nimepigana na Raba,+ nami nimeliteka jiji lenye maji.* 28 Sasa wakusanye wanajeshi waliobaki, upige kambi dhidi ya jiji hilo na kuliteka. La sivyo, mimi ndiye nitakayeliteka jiji hilo, na kusifiwa kwa kuliteka.”*

29 Basi Daudi akawakusanya wanajeshi wote na kwenda Raba, akapigana nalo na kuliteka. 30 Kisha akachukua taji lililokuwa kwenye kichwa cha Malkamu. Uzito wa taji hilo ulikuwa talanta moja* ya dhahabu, nalo lilikuwa na mawe yenye thamani, Daudi akavishwa taji hilo kichwani. Alichukua pia nyara nyingi sana+ kutoka katika jiji hilo.+ 31 Akawatoa nje watu waliokuwa ndani yake, akawapa kazi ya kukata mawe kwa misumeno, vifaa vya chuma vyenye ncha kali na mashoka ya chuma, na kazi ya kufyatua matofali. Hivyo ndivyo alivyofanya katika majiji yote ya Waamoni. Hatimaye Daudi na wanajeshi wote wakarudi Yerusalemu.

13 Sasa Absalomu mwana wa Daudi alikuwa na dada mrembo aliyeitwa Tamari,+ basi Amnoni+ mwana wa Daudi akampenda. 2 Amnoni akateseka sana hivi kwamba akawa mgonjwa kwa sababu ya Tamari dada yake, kwa maana alikuwa bikira na ilionekana kwamba haiwezekani kwa Amnoni kumfanyia jambo lolote. 3 Sasa Amnoni alikuwa na rafiki aliyeitwa Yehonadabu,+ mwana wa Shimea,+ ndugu ya Daudi; na Yehonadabu alikuwa mtu mjanja sana. 4 Kwa hiyo akamuuliza: “Kwa nini wewe, mwana wa mfalme, unasononeka kila asubuhi? Kwa nini usiniambie?” Amnoni akamjibu hivi: “Ninampenda Tamari, dada+ ya ndugu yangu Absalomu.” 5 Yehonadabu akamwambia: “Lala kitandani mwako, ujifanye mgonjwa. Baba yako akija kukuona, mwambie, ‘Tafadhali, mruhusu dada yangu Tamari aje kuniandalia chakula kidogo. Akitayarisha chakula cha mgonjwa* mbele ya macho yangu nitakichukua kutoka mkononi mwake na kula.’”

6 Basi Amnoni akalala kitandani na kujifanya mgonjwa, hivyo mfalme akaja kumwona. Ndipo Amnoni akamwambia mfalme: “Tafadhali, mruhusu dada yangu Tamari aje kuniokea keki mbili zenye umbo la moyo mbele ya macho yangu, ili nichukue chakula kutoka mkononi mwake.” 7 Kwa hiyo Daudi akamtumia Tamari ujumbe nyumbani, akisema: “Tafadhali, nenda katika nyumba ya ndugu yako Amnoni, umtayarishie chakula.”* 8 Basi Tamari akaenda katika nyumba ya ndugu yake Amnoni, alimokuwa amelala. Akachukua unga, akaukanda na kuoka keki mbele ya Amnoni. 9 Kisha akachukua kikaango na kumpa keki hizo. Lakini Amnoni akakataa kula, akasema: “Waambie watu wote waondoke!” Basi watu wote wakaondoka.

10 Kisha Amnoni akamwambia Tamari: “Niletee chakula* katika chumba cha kulala, ili nikichukue kutoka mkononi mwako na kukila.” Basi Tamari akachukua keki zenye umbo la moyo ambazo alikuwa ameoka na kumletea Amnoni ndugu yake katika chumba cha kulala. 11 Alipomletea ili ale, Amnoni akamkamata kwa nguvu na kumwambia: “Njoo, ulale nami, dada yangu.” 12 Lakini Tamari akamwambia: “Usifanye hivyo ndugu yangu! Usiniabishe, kwa maana jambo kama hili halipaswi kufanywa katika Israeli.+ Usitende jambo hili la aibu.+ 13 Nitaondoaje aibu yangu? Nawe utaonwa kuwa kama mmojawapo wa wanaume wapumbavu katika Israeli. Sasa, tafadhali, ongea na mfalme, kwa maana hatakukataza unichukue.” 14 Lakini Amnoni akakataa kumsikiliza, akamzidi nguvu Tamari na kumwaibisha kwa kumbaka. 15 Kisha Amnoni akaanza kumchukia kwa chuki kali sana, hivi kwamba chuki hiyo ikawa kubwa sana kuliko upendo aliokuwa nao mwanzoni kumwelekea. Amnoni akamwambia: “Inuka; nenda zako!” 16 Ndipo Tamari akamwambia: “Usinifukuze, ndugu yangu, kwa maana kitendo cha kunifukuza sasa ni kibaya zaidi kuliko jambo ulilonitendea!” Lakini Amnoni akakataa kumsikiliza.

17 Basi akamwita kijana aliyemtumikia na kumwambia: “Tafadhali, mwondoe mtu huyu mbele yangu, na ufunge mlango.” 18 (Sasa Tamari alikuwa amevaa joho la pekee,* kwa maana hayo ndiyo mavazi yaliyovaliwa na mabinti wa mfalme waliokuwa mabikira.) Kwa hiyo mtumishi huyo akamtoa nje na kufunga mlango. 19 Tamari akatia majivu kichwani mwake,+ akalirarua joho bora alilokuwa amevaa; akaweka mikono yake kichwani na kwenda zake, huku akilia kwa sauti alipokuwa akitembea.

20 Ndipo Absalomu ndugu yake+ akamuuliza: “Je, ni Amnoni ndugu yako aliyelala nawe? Sasa nyamaza, dada yangu. Yeye ni ndugu yako.+ Usiruhusu jambo hili likae moyoni mwako.” Hivyo, Tamari akaishi peke yake katika nyumba ya Absalomu ndugu yake. 21 Mfalme Daudi aliposikia mambo hayo yote, alikasirika sana.+ Lakini hakutaka kumuumiza hisia Amnoni mwanawe, kwa sababu alimpenda, na alikuwa mzaliwa wake wa kwanza. 22 Absalomu hakumwambia Amnoni jambo lolote jema au baya; kwa maana Absalomu alimchukia+ Amnoni kwa sababu alikuwa amemwaibisha Tamari dada yake.+

23 Baada ya miaka miwili kamili, wakataji manyoya ya kondoo wa Absalomu walipokuwa kule Baal-hasori, karibu na Efraimu,+ Absalomu aliwaalika wana wote wa mfalme.+ 24 Basi Absalomu akaja kwa mfalme na kumwambia: “Kondoo wangu, mimi mtumishi wako, wanakatwa manyoya. Nakuomba wewe mfalme na watumishi wako twende pamoja.” 25 Lakini mfalme akamwambia Absalomu: “La, mwanangu. Tukienda sisi sote, tutakuwa mzigo kwako.” Ingawa aliendelea kumsihi, mfalme hakukubali kwenda, lakini alimbariki. 26 Ndipo Absalomu akamwambia: “Ikiwa hutaenda, tafadhali mruhusu Amnoni ndugu yangu aende pamoja nasi.”+ Mfalme akamuuliza: “Kwa nini aende pamoja nawe?” 27 Lakini Absalomu akamsihi, kwa hiyo mfalme akamruhusu Amnoni na wana wote wa mfalme waende pamoja na Absalomu.

28 Kisha Absalomu akawaagiza hivi watumishi wake: “Mwangalieni Amnoni, moyo wake utakapokuwa umechangamka kwa sababu ya divai, nitawaambia, ‘Muueni Amnoni!’ Ndipo mtakapomuua. Msiogope. Je, si mimi ndiye huwaamuru? Iweni imara na jasiri.” 29 Basi watumishi wa Absalomu wakamtendea Amnoni kama Absalomu alivyowaagiza; kisha wana wale wengine wa mfalme wakainuka, na kila mmoja wao akapanda nyumbu wake na kukimbia. 30 Walipokuwa njiani, habari hii ikamfikia Daudi: “Absalomu amewaua wana wote wa mfalme, na hakuna hata mmoja aliyebaki hai.” 31 Ndipo mfalme akasimama, akararua mavazi yake, na kulala chini, nao watumishi wake wote walikuwa wamesimama kando yake na mavazi yao yalikuwa yameraruliwa.

32 Hata hivyo, Yehonadabu+ mwana wa Shimea,+ ndugu ya Daudi, akasema: “Bwana wangu usifikiri kwamba wamewaua wana wote wa mfalme, kwa maana Amnoni peke yake ndiye aliyekufa.+ Absalomu ndiye aliyeagiza auawe kwa sababu alikuwa amekusudia kufanya hivyo+ tangu Amnoni alipomwaibisha Tamari+ dada yake.+ 33 Sasa bwana wangu mfalme usisikilize habari hii inayosema, ‘Wana wote wa mfalme wamekufa’; ni Amnoni peke yake aliyekufa.”

34 Wakati huo, Absalomu akakimbia.+ Baadaye mlinzi akainua macho yake, akaona watu wengi wakija barabarani nyuma yake kando ya mlima. 35 Ndipo Yehonadabu+ akamwambia mfalme: “Tazama! Wana wa mfalme wamerudi, kama tu nilivyokwambia mimi mtumishi wako.” 36 Mara tu alipomaliza kuzungumza, wana wa mfalme wakaingia, wakilia kwa sauti; mfalme pia na watumishi wake wote wakalia kwa uchungu sana. 37 Lakini Absalomu akakimbia na kwenda kwa Talmai+ mwana wa Amihudi mfalme wa Geshuri. Daudi akamwombolezea mwana wake kwa siku nyingi. 38 Absalomu alipokimbia na kwenda Geshuri,+ alikaa huko kwa miaka mitatu.

39 Mwishowe Mfalme Daudi akatamani kwenda kumwona Absalomu, kwa maana alikuwa ametulia* baada ya kifo cha Amnoni.

14 Sasa Yoabu mwana wa Seruya+ akatambua kwamba moyo wa mfalme ulitamani kumwona Absalomu.+ 2 Kwa hiyo Yoabu akatuma watu huko Tekoa+ wamlete mwanamke mwerevu, akamwambia hivi: “Tafadhali, jifanye kana kwamba unaomboleza, nawe uvae nguo za kuomboleza, na usijipake mafuta.+ Jifanye kama mwanamke ambaye amekuwa akiomboleza kwa siku nyingi kwa sababu ya kufiwa. 3 Kisha uende kwa mfalme na kumwambia hivi.” Basi Yoabu akamwambia mambo ya kusema.*

4 Mwanamke huyo Mtekoa akaenda kwa mfalme, akaanguka chini kifudifudi, akainama na kusema: “Ee mfalme, nisaidie!” 5 Mfalme akamuuliza: “Kuna shida gani?” Mwanamke huyo akasema: “Mimi ni mjane; mume wangu amekufa. 6 Nami, mtumishi wako, nilikuwa na wana wawili, nao wakapigana walipokuwa shambani. Hapakuwa na mtu wa kuwatenganisha, mwana mmoja akampiga mwenzake na kumuua. 7 Sasa watu wote wa familia wako dhidi yangu, mimi mtumishi wako, nao wanasema, ‘Mtoe yule aliyemuua ndugu yake, ili tumuue kwa sababu ya uhai wa* ndugu yake ambaye alimuua,+ hata kama tutamwangamiza mrithi wake!’ Watakuwa wamezima kaa langu la mwisho linalowaka,* na mume wangu hatakuwa na jina wala mzao* duniani.”

8 Ndipo mfalme akamwambia mwanamke huyo: “Nenda nyumbani kwako, nami nitatoa agizo kukuhusu.” 9 Mwanamke huyo Mtekoa akamwambia mfalme: “Ee bwana wangu mfalme, hatia na iwe juu yangu na juu ya nyumba ya baba yangu, lakini wewe mfalme na kiti chako cha ufalme hakina hatia.” 10 Mfalme akamwambia: “Mtu yeyote akizungumza nawe tena, mlete kwangu, naye hatakusumbua tena kamwe.” 11 Lakini mwanamke huyo akasema: “Tafadhali mfalme, mkumbuke Yehova Mungu wako, ili mtu anayelipiza kisasi cha damu+ asilete maangamizi zaidi kwa kumuua mwanangu.” Mfalme akasema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi,+ hakuna hata unywele mmoja wa mwana wako utakaoanguka chini.” 12 Ndipo mwanamke huyo akasema: “Tafadhali, niruhusu mimi mtumishi wako, nikwambie neno moja, bwana wangu mfalme.” Basi mfalme akasema: “Niambie!”

13 Mwanamke huyo akasema: “Kwa nini, basi, umefikiria kuwatendea watu wa Mungu jambo kama hilo?+ Mfalme akisema jambo kama hilo, anajitia katika hatia, kwa sababu mfalme hamrudishi mwana wake aliyefukuzwa.+ 14 Hakika tutakufa na kuwa kama maji yanayomwagwa chini, ambayo hayawezi kuzolewa. Lakini Mungu haondoi uhai,* naye hufikiria sababu za kumrudisha yule aliyefukuzwa. 15 Nimekuja kukwambia jambo hili bwana wangu mfalme kwa sababu watu walinitia woga. Basi mimi mtumishi wako nikasema, ‘Tafadhali, niruhusu nizungumze na mfalme. Huenda mfalme atatimiza ombi langu, mimi mtumwa wake. 16 Huenda mfalme akasikiliza na kuniokoa mimi mtumwa wake kutoka mikononi mwa mtu anayetaka kuniangamiza mimi na mwanangu wa pekee kutoka kwa urithi ambao Mungu alitupatia.’+ 17 Kisha mimi mtumishi wako nikasema, ‘Acha neno la bwana wangu mfalme linitulize,’ kwa maana bwana wangu mfalme ni kama malaika wa Mungu wa kweli katika kutofautisha jambo lililo jema na lililo baya. Yehova Mungu wako awe pamoja nawe.”

18 Basi mfalme akamwambia mwanamke huyo: “Tafadhali, usinifiche jambo lolote nitakalokuuliza.” Mwanamke huyo akamwambia: “Tafadhali, sema bwana wangu mfalme.” 19 Basi mfalme akamuuliza: “Je, Yoabu ndiye aliyekuambia ufanye hivi?”+ Mwanamke huyo akajibu: “Kwa hakika kama unavyoishi, Ee bwana wangu mfalme, ni kama tu ulivyosema bwana wangu mfalme, kwa kuwa Yoabu mtumishi wako ndiye aliyeniagiza mimi mtumishi wako na kuniambia niseme maneno hayo yote.* 20 Mtumishi wako Yoabu amefanya hivyo ili mambo yaonekane tofauti, lakini wewe bwana wangu una hekima kama ya malaika wa Mungu wa kweli na unajua mambo yote yanayotendeka nchini.”

21 Basi mfalme akamwambia Yoabu: “Sawa, nitafanya jambo hilo.+ Nenda ukamlete kijana Absalomu.”+ 22 Ndipo Yoabu akaanguka chini kifudifudi, akainama na kumsifu mfalme. Yoabu akasema: “Leo mimi mtumishi wako ninajua kwamba nimepata kibali machoni pako, Ee bwana wangu mfalme, kwa maana wewe mfalme umetimiza ombi langu, mimi mtumishi wako.” 23 Kisha Yoabu akaondoka kwenda Geshuri+ na kumleta Absalomu Yerusalemu. 24 Hata hivyo, mfalme akasema: “Acha arudi nyumbani kwake, lakini hatauona uso wangu.” Basi Absalomu akarudi nyumbani kwake, naye hakuuona uso wa mfalme.

25 Sasa katika Israeli yote, hakuna mwanamume yeyote aliyesifiwa kwa sura yake nzuri kama Absalomu. Hakuwa na kasoro yoyote, kuanzia wayo wa mguu mpaka utosi wa kichwa chake. 26 Aliponyoa kichwa chake—kwa maana alikinyoa mwishoni mwa kila mwaka kwa sababu nywele zake zilikuwa nzito sana—nywele hizo zilikuwa na uzito wa shekeli 200* kulingana na mizani ya kifalme.* 27 Absalomu alizaa wana watatu+ na binti mmoja ambaye aliitwa Tamari. Alikuwa mwanamke mrembo sana.

28 Absalomu akaendelea kuishi Yerusalemu kwa miaka miwili kamili, lakini hakuuona uso wa mfalme.+ 29 Basi Absalomu akamwita Yoabu ili amtume kwa mfalme, lakini Yoabu akakataa kuja. Kisha akatuma mtu amwite kwa mara ya pili, lakini bado akakataa kuja. 30 Mwishowe akawaambia watumishi wake: “Shamba la Yoabu liko kando ya shamba langu, nalo lina shayiri. Nendeni mkalichome moto.” Basi watumishi wa Absalomu wakalichoma moto shamba hilo. 31 Yoabu akaenda nyumbani kwa Absalomu na kumuuliza: “Kwa nini watumishi wako walilichoma moto shamba langu?” 32 Absalomu akamjibu Yoabu: “Tazama! nilikutumia ujumbe huu, ‘Njoo nikutume kwa mfalme, umuulize: “Kwa nini niliondoka Geshuri?+ Afadhali ningekaa huko. Sasa acha nikauone uso wa mfalme, na ikiwa nina hatia, basi aniue.”’”

33 Kwa hiyo Yoabu akaenda kwa mfalme na kumwambia. Kisha akamwita Absalomu, naye akaja kwa mfalme na kuanguka chini kifudifudi, mbele ya mfalme. Kisha mfalme akambusu Absalomu.+

15 Baada ya mambo hayo yote, Absalomu akajipatia gari na farasi na watu 50 wa kukimbia mbele yake.+ 2 Absalomu alikuwa akiamka mapema na kusimama kando ya barabara iliyoelekea kwenye lango la jiji.+ Absalomu alikuwa akimwita na kumuuliza hivi mtu yeyote aliyekuwa na kesi ambayo ilipaswa kuamuliwa na mfalme:+ “Unatoka jiji gani?” naye alijibu: “Mimi mtumishi wako ninatoka katika mojawapo ya makabila ya Waisraeli.” 3 Kisha Absalomu alimwambia: “Madai yako ni ya kweli na ya haki, lakini hakuna yeyote kutoka kwa mfalme wa kusikiliza kesi yako.” 4 Absalomu alimwambia: “Laiti ningewekwa kuwa mwamuzi nchini! Kila mtu aliye na kesi au mashtaka angekuja kwangu, nami ningehakikisha kwamba anatendewa haki.”

5 Mtu alipomkaribia ili amwinamie, Absalomu alikuwa akinyoosha mkono wake na kumshika na kumbusu.+ 6 Absalomu alikuwa akiwafanyia hivyo Waisraeli wote waliokuwa wakienda kwa mfalme kuwasilisha mashtaka yao; basi Absalomu akaendelea kuiba mioyo ya Waisraeli.+

7 Mwishoni mwa miaka minne,* Absalomu akamwambia mfalme: “Tafadhali, acha niende Hebroni+ nikatimize nadhiri yangu niliyomwekea Yehova. 8 Kwa maana mimi mtumishi wako nilipokuwa nikiishi Geshuri+ huko Siria niliweka nadhiri hii takatifu:+ ‘Ikiwa Yehova atanirudisha Yerusalemu, nitamtolea Yehova dhabihu.’”* 9 Basi mfalme akamwambia: “Nenda kwa amani.” Absalomu akaondoka na kwenda Hebroni.

10 Sasa Absalomu akawatuma wapelelezi katika makabila yote ya Israeli, akawaambia: “Mara tu mtakaposikia sauti ya pembe, tangazeni hivi: ‘Absalomu amekuwa mfalme katika Hebroni!’”+ 11 Absalomu alikuwa ameenda huko na wanaume 200 kutoka Yerusalemu; alikuwa amewakaribisha, nao hawakushuku wala kujua kilichokuwa kikiendelea. 12 Isitoshe, Absalomu alipotoa dhabihu, aliwatuma watu wamwite Ahithofeli+ Mgiloni, mshauri wa Daudi,+ kutoka jiji la Gilo.+ Njama iliendelea kupamba moto, na idadi ya watu waliomuunga mkono Absalomu ikaendelea kuongezeka.+

13 Baada ya muda mpelelezi fulani akaja kwa Daudi na kumwambia: “Mioyo ya watu wa Israeli imegeuka kumfuata Absalomu.” 14 Mara moja Daudi akawaambia watumishi wake wote waliokuwa pamoja naye huko Yerusalemu: “Tuondoke, tukimbie,+ kwa maana hakuna yeyote kati yetu atakayemkwepa Absalomu! Fanyeni haraka, asije akatufikia na kutuletea msiba na kuwaua watu wote jijini kwa upanga!”+ 15 Watumishi wa mfalme wakamwambia mfalme: “Lolote ambalo wewe bwana wetu mfalme utaamua, sisi watumishi wako tuko tayari kulifanya.”+ 16 Basi mfalme akatoka pamoja na watu wote wa nyumbani mwake, lakini mfalme akawaacha masuria kumi+ ili watunze nyumba.* 17 Mfalme akaondoka pamoja na watu wote waliokuwa pamoja naye, wakasimama Beth-merhaki.

18 Watumishi wake wote walioondoka pamoja naye* na Wakerethi wote na Wapelethi+ wote na Wagathi+ wote, watu 600 waliokuwa wamemfuata kutoka Gathi,+ wakapita mbele yake akiwachunguza.* 19 Ndipo mfalme akamwambia Itai+ Mgathi: “Kwa nini wewe pia uende pamoja nasi? Rudi ukaishi na mfalme mpya, kwa sababu wewe ni mgeni, na pia ulifukuzwa kutoka katika nchi yako. 20 Ulikuja jana tu, kwa nini leo nikufanye utange-tange pamoja nasi, uende wakati ninapohitaji kwenda na mahali popote ninapoenda? Rudi pamoja na ndugu zako, na Yehova akutendee kwa upendo mshikamanifu na kwa uaminifu!”+ 21 Lakini Itai akamwambia mfalme: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi na kwa hakika kama bwana wangu mfalme anavyoishi, mahali popote utakapokuwa wewe bwana wangu mfalme, ukiwa hai au ukiwa umekufa, mimi mtumishi wako nitakuwa mahali hapo!”+ 22 Ndipo Daudi akamwambia Itai:+ “Pita uvuke.” Basi Itai Mgathi akavuka, pamoja na watu wake wote na watoto wake.

23 Watu wote nchini walikuwa wakilia kwa sauti kubwa watu hao wote walipokuwa wakivuka ng’ambo ile nyingine, naye mfalme alikuwa amesimama kando ya Bonde la Kidroni;+ watu wote walivuka na kufuata barabara inayoelekea nyikani. 24 Sadoki+ pia alikuwa mahali hapo pamoja na Walawi wote+ waliobeba sanduku+ la agano la Mungu wa kweli;+ nao wakaliweka chini Sanduku la Mungu wa kweli; Abiathari+ pia alikuwepo watu wote walipovuka kutoka jijini. 25 Lakini mfalme akamwambia Sadoki: “Lirudishe jijini Sanduku la Mungu wa kweli.+ Nikipata kibali machoni pa Yehova, atanirudisha na kuniruhusu kuliona na kuona mahali linapokaa.+ 26 Lakini akisema, ‘Sipendezwi nawe,’ basi na anitendee jambo lolote analoona ni jema.” 27 Mfalme akamwambia kuhani Sadoki: “Je, wewe si mwonaji?+ Rudi jijini kwa amani, na pia wachukue wana wenu wawili, Ahimaazi mwana wako na Yonathani+ mwana wa Abiathari. 28 Nitangojea kando ya vivuko vya nyikani mpaka nitakapopata habari kutoka kwenu.”+ 29 Basi Sadoki na Abiathari wakalirudisha Sanduku la Mungu wa kweli Yerusalemu, nao wakabaki huko.

30 Daudi alipanda Mlima wa Mizeituni+ huku akilia; alikuwa amefunika kichwa chake, na alikuwa miguu mitupu. Pia watu wote waliokuwa pamoja naye walifunika vichwa vyao, nao walikuwa wakilia huku wakipanda. 31 Kisha Daudi akaambiwa hivi: “Ahithofeli ni miongoni mwa watu wanaopanga njama+ pamoja na Absalomu.”+ Daudi akasema: “Ee Yehova,+ tafadhali badili ushauri wa Ahithofeli uwe upumbavu!”+

32 Daudi alipofika kwenye kilele, mahali ambapo watu walizoea kumwinamia Mungu, Hushai+ Mwarki+ alikuwa mahali hapo ili kumpokea, joho lake lilikuwa limeraruka na alikuwa na mavumbi kichwani. 33 Hata hivyo, Daudi akamwambia: “Ukivuka kwenda pamoja nami, utakuwa mzigo kwangu. 34 Lakini ukirudi jijini nawe umwambie Absalomu, ‘Mimi ni mtumishi wako, Ee mfalme. Nilikuwa mtumishi wa baba yako zamani, lakini sasa mimi ni mtumishi wako,’+ ndipo utakaponisaidia kuvuruga ushauri wa Ahithofeli.+ 35 Kuhani Sadoki na Abiathari wako huko pamoja nawe. Utamwambia kuhani Sadoki na Abiathari mambo yote utakayosikia katika nyumba ya mfalme.+ 36 Wana wao wawili, Ahimaazi+ mwana wa Sadoki na Yonathani+ mwana wa Abiathari wako huko pamoja nao, nanyi mtawatumia wana hao kuniletea habari zote mtakazosikia.” 37 Basi Hushai rafiki ya*+ Daudi akaingia jijini Absalomu alipokuwa akiingia Yerusalemu.

16 Daudi alipokuwa amepita mbele kidogo ya kile kilele,+ Siba+ mtumishi wa Mefiboshethi+ alikuwa hapo ili kumpokea; alikuwa na punda wawili wenye matandiko, na walikuwa wamebeba mikate 200, keki 100 za zabibu kavu, keki 100 za matunda ya kiangazi,* na mtungi mkubwa wa divai.+ 2 Mfalme akamuuliza Siba: “Kwa nini umeleta vitu hivi?” Siba akamjibu: “Punda ni kwa ajili ya nyumba ya mfalme ili wapande juu yao, mikate na matunda ya kiangazi ni kwa ajili ya vijana, na divai ni kwa ajili ya wale watakaochoka nyikani.”+ 3 Mfalme akamuuliza: “Na mwana wa bwana wako yuko wapi?”+ Siba akamwambia mfalme: “Yuko Yerusalemu, kwa maana alisema, ‘Leo nyumba ya Israeli itanirudishia utawala wa kifalme wa baba yangu.’”+ 4 Ndipo mfalme akamwambia Siba: “Tazama! Mali yote ya Mefiboshethi ni yako.”+ Siba akasema: “Nainama mbele yako. Acha nipate kibali machoni pako, bwana wangu mfalme.”+

5 Mfalme Daudi alipofika Bahurimu, mtu fulani kutoka katika ukoo wa nyumba ya Sauli anayeitwa Shimei,+ mwana wa Gera, akaja kumtukana Daudi huku akimkaribia.+ 6 Alikuwa akimtupia Daudi mawe, na watumishi wote wa Mfalme Daudi, pamoja na watu wote na wanaume mashujaa waliokuwa upande wake wa kulia na wa kushoto. 7 Shimei alimtukana akisema: “Ondoka, ondoka, wewe mtu mwenye hatia ya damu! Wewe mtu asiyefaa kitu! 8 Yehova amekulipiza kwa sababu ya hatia yote uliyopata kwa kumwaga damu ya watu wa nyumba ya Sauli, ambaye umechukua mahali pake na kutawala ukiwa mfalme, lakini Yehova anautia ufalme mikononi mwa Absalomu mwana wako. Sasa msiba umekupata kwa sababu wewe ni mtu mwenye hatia ya damu!”+

9 Ndipo Abishai mwana wa Seruya+ akamwambia mfalme: “Kwa nini huyu mbwa mfu+ akutukane bwana wangu mfalme?+ Tafadhali niruhusu nivuke, nikamkate kichwa.”+ 10 Lakini mfalme akasema: “Nina nini nanyi, enyi wana wa Seruya?+ Mwacheni anitukane,+ kwa sababu Yehova amemwambia,+ ‘Mtukane Daudi!’ Basi ni nani anayepaswa kumuuliza, ‘Kwa nini unafanya hivi?’” 11 Kisha Daudi akamwambia Abishai na watumishi wake wote: “Ikiwa mwanangu mwenyewe, niliyemzaa anatafuta uhai wangu,*+ je, Mbenjamini hatafanya zaidi?+ Mwacheni anitukane, kwa maana Yehova alimwambia afanye hivyo! 12 Huenda Yehova ataona mateso yangu,+ na Yehova atanilipa kwa wema badala ya matusi niliyotukanwa leo hii.”+ 13 Kwa hiyo Daudi na wanaume wake wakaendelea kuteremka barabarani huku Shimei akitembea kando ya mlima sambamba na Daudi, naye alikuwa akimtukana kwa sauti,+ akitupa mawe na kurusha mavumbi mengi.

14 Hatimaye mfalme na watu wote waliokuwa pamoja naye wakafika wakiwa wamechoka mahali walikokuwa wakienda, nao wakapumzika.*

15 Wakati huo, Absalomu na wanaume wote wa Israeli wakafika Yerusalemu, na Ahithofeli+ alikuwa pamoja naye. 16 Hushai+ Mwarki,+ rafiki ya* Daudi, alipoingia kwa Absalomu, alimwambia hivi Absalomu: “Mfalme na aishi muda mrefu!+ Mfalme na aishi muda mrefu!” 17 Ndipo Absalomu akamuuliza Hushai: “Je, huu ndio upendo mshikamanifu unaomtendea rafiki yako? Kwa nini hukwenda na rafiki yako?” 18 Basi Hushai akamwambia Absalomu: “Siwezi kufanya hivyo, ninamuunga mkono yule aliyechaguliwa na Yehova, na watu hawa, na wanaume wote wa Israeli. Nitakaa pamoja naye. 19 Na kwa mara nyingine nasema, Ninapaswa kumtumikia nani? Je, sipaswi kumtumikia mwana wake? Kama nilivyomtumikia baba yako, ndivyo nitakavyokutumikia.”+

20 Ndipo Absalomu akamwambia Ahithofeli: “Nipe ushauri.+ Tufanye nini?” 21 Basi Ahithofeli akamwambia Absalomu: “Fanya ngono na masuria wa baba yako,+ aliowaacha waitunze nyumba.*+ Kisha Waisraeli wote watasikia kwamba umekuwa uvundo kwa baba yako, na wale wanaokuunga mkono watapata nguvu.” 22 Kwa hiyo wakampigia hema Absalomu juu ya paa,+ naye Absalomu akafanya ngono na masuria wa baba yake+ Waisraeli wote wakitazama.+

23 Siku hizo, ushauri uliotolewa na Ahithofeli+ ulionwa kama neno la* Mungu wa kweli. Hivyo ndivyo ushauri wote wa Ahithofeli ulivyothaminiwa, na Daudi na pia Absalomu.

17 Kisha Ahithofeli akamwambia Absalomu: “Tafadhali, niruhusu nichague wanaume 12,000 niende kumfuatia Daudi usiku wa leo. 2 Nitamkuta akiwa amechoka na akiwa dhaifu,*+ kisha nitamtia woga; na watu wote walio pamoja naye watakimbia, nami nitamuua mfalme peke yake.+ 3 Halafu nitawarudisha watu wote kwako. Kurudi kwa watu wote kunategemea kitakachompata mtu unayemtafuta. Kisha watu wote watakuwa na amani.” 4 Pendekezo hilo lilikuwa zuri kabisa machoni pa Absalomu na wazee wote wa Israeli.

5 Hata hivyo, Absalomu akasema: “Tafadhali, mwiteni pia Hushai+ Mwarki, tusikie jambo atakalosema.” 6 Basi Hushai akaja kwa Absalomu. Kisha Absalomu akamwambia: “Huu ndio ushauri uliotolewa na Ahithofeli. Je, tufuate ushauri wake? Kama sivyo, tuambie jambo la kufanya.” 7 Ndipo Hushai akamwambia Absalomu: “Wakati huu, ushauri uliotolewa na Ahithofeli si mzuri!”+

8 Hushai akaendelea kusema: “Unajua vizuri kwamba baba yako na wanaume wake ni mashujaa,+ na wana hasira* kama dubu aliyepoteza watoto wake porini.+ Isitoshe, baba yako ni mpiganaji hodari,+ naye hatakaa usiku kucha na watu. 9 Sasa hivi amejificha ndani ya mojawapo ya mapango* au mahali pengine;+ ikiwa atakuwa wa kwanza kutushambulia, wale watakaosikia habari hiyo watasema, ‘Watu wanaomfuata Absalomu wameshindwa!’ 10 Hata mwanamume jasiri aliye na moyo kama wa simba+ hakika atanyong’onyea kwa woga, kwa maana Waisraeli wote wanajua kwamba baba yako ni mwanamume shujaa+ na kwamba wanaume walio pamoja naye ni jasiri. 11 Natoa ushauri huu: Waisraeli wote na wakusanyike kwako, kuanzia Dani mpaka Beer-sheba,+ wengi kama chembe za mchanga kwenye ufuo wa bahari,+ nawe uwaongoze vitani. 12 Tutamshambulia mahali popote atakapopatikana, nasi tutamwangukia kama umande unavyoanguka ardhini; na hakuna hata mmoja wao atakayeokoka, wala yeye wala mwanamume yeyote aliye pamoja naye. 13 Ikiwa atakimbilia jiji fulani, Waisraeli wote watachukua kamba na kwenda katika jiji hilo na kuliburuta mpaka bondeni, na hakuna hata jiwe dogo litakalobaki.”

14 Ndipo Absalomu na wanaume wote wa Israeli wakasema: “Ushauri wa Hushai Mwarki ni bora+ kuliko ushauri wa Ahithofeli!” Kwa maana Yehova alikuwa ameazimia* kuvuruga ushauri mzuri wa Ahithofeli,+ ili Yehova amletee msiba Absalomu.+

15 Baadaye Hushai akamwambia Sadoki na Abiathari+ waliokuwa makuhani: “Hivi ndivyo Ahithofeli alivyomshauri Absalomu na wazee wa Israeli, na hivi ndivyo nilivyowashauri. 16 Sasa tumeni ujumbe haraka kwa Daudi na kumwonya hivi: ‘Usikae kwenye vivuko vilivyo nyikani usiku wa leo, lakini hakikisha umevuka, usipofanya hivyo, wewe mfalme na watu wote walio pamoja nawe mtaangamizwa.’”*+

17 Yonathani+ na Ahimaazi+ walikuwa wakikaa En-rogeli;+ basi kijakazi fulani akaenda na kuwaambia, nao wakaenda kumwambia Mfalme Daudi kwa maana hawakutaka kujihatarisha kwa kuonekana wakiingia jijini. 18 Hata hivyo, kijana fulani akawaona na kumwambia Absalomu. Basi wote wawili wakaondoka haraka na kwenda mpaka kwenye nyumba ya mtu fulani huko Bahurimu+ aliyekuwa na kisima katika ua wa nyumba yake. Wakaingia kisimani, 19 kisha mke wa mwanamume huyo akakifunika kisima hicho na kuweka chengachenga za nafaka juu yake; hakuna aliyejua jambo hilo. 20 Watumishi wa Absalomu wakaja kwa mwanamke huyo nyumbani kwake na kumuuliza: “Ahimaazi na Yonathani wako wapi?” Mwanamke huyo akawajibu: “Walipita hapa wakaenda kwenye maji.”+ Kisha wanaume hao wakawatafuta lakini hawakuwapata, basi wakarudi Yerusalemu.

21 Baada ya wanaume hao kwenda zao, walitoka kisimani na kwenda kumjulisha Mfalme Daudi. Wakamwambia: “Ondoka, uvuke haraka maji haya, kwa maana Ahithofeli ametoa ushauri dhidi yako.”+ 22 Mara moja Daudi na watu wote waliokuwa pamoja naye wakaondoka na kuvuka Yordani. Wakati wa mapambazuko, hapakuwa na mtu hata mmoja ambaye hakuwa amevuka Yordani.

23 Ahithofeli alipoona kwamba ushauri wake haukufuatwa, aliweka matandiko juu ya punda wake na kwenda nyumbani kwake katika mji wao.+ Baada ya kuwapa maagizo watu wa nyumbani mwake,+ akajitia kitanzi.*+ Basi akafa na kuzikwa katika makaburi ya mababu zake.

24 Wakati huo, Daudi akaenda Mahanaimu,+ naye Absalomu akavuka Yordani pamoja na wanaume wote wa Israeli. 25 Absalomu alimweka Amasa+ kuwa msimamizi wa jeshi badala ya Yoabu;+ Amasa alikuwa mwana wa mwanamume Mwisraeli aliyeitwa Ithra, aliyelala na Abigaili,+ binti ya Nahashi, dada ya Seruya, mama ya Yoabu. 26 Waisraeli na Absalomu wakapiga kambi katika nchi ya Gileadi.+

27 Mara tu Daudi alipofika Mahanaimu, Shobi mwana wa Nahashi kutoka katika jiji la Raba+ la Waamoni, Makiri+ mwana wa Amieli kutoka Lo-debari, na Barzilai+ Mgileadi kutoka Rogelimu 28 wakaleta vitanda, mabeseni, vyungu, ngano, shayiri, unga, nafaka iliyokaangwa, maharagwe mapana, dengu, nafaka iliyokauka, 29 asali, siagi, kondoo, na jibini. Walimletea vitu hivyo vyote Daudi na watu waliokuwa pamoja naye ili wale,+ kwa maana walisema: “Watu wana njaa, wamechoka, na wana kiu nyikani.”+

18 Kisha Daudi akawahesabu watu waliokuwa pamoja naye na kuweka juu yao wakuu wa maelfu na wakuu wa mamia.+ 2 Na Daudi akatuma theluthi ya wanaume chini ya amri ya* Yoabu,+ na theluthi nyingine chini ya amri ya Abishai+ mwana wa Seruya,+ ndugu ya Yoabu, na theluthi nyingine chini ya amri ya Itai+ Mgathi. Kisha mfalme akawaambia wanaume hao: “Mimi pia nitaenda pamoja nanyi.” 3 Lakini wakasema: “Usiende,+ kwa maana tukikimbia, hawatashughulika nasi;* na nusu yetu tukifa, hawatajali juu yetu, kwa maana thamani yako ni sawa na watu 10,000 miongoni mwetu.+ Kwa hiyo, litakuwa jambo bora zaidi ikiwa utatutumia msaada kutoka jijini.” 4 Mfalme akawaambia: “Nitafanya jambo lolote mnaloona ni jema zaidi.” Kwa hiyo mfalme akasimama karibu na lango la jiji na wanaume wote wakatoka wakiwa katika makundi ya mamia na maelfu. 5 Kisha mfalme akampa agizo hili Yoabu, Abishai, na Itai: “Mtendeeni kwa upole kijana Absalomu kwa ajili yangu.”+ Wanaume wote walimsikia mfalme akiwapa wakuu wote agizo hilo kuhusu Absalomu.

6 Wanaume hao wakaenda kupigana na Waisraeli, walipigana vita hivyo katika msitu wa Efraimu.+ 7 Huko, watu wa Israeli+ wakashindwa na watumishi wa Daudi,+ na wanaume wengi wakauawa siku hiyo—wanaume 20,000. 8 Vita vikaenea katika eneo lote. Isitoshe, msitu uliwaua* watu wengi zaidi kuliko waliouawa kwa upanga siku hiyo.

9 Mwishowe Absalomu akakutana kwa ghafla na watumishi wa Daudi. Absalomu alikuwa amepanda juu ya nyumbu, na nyumbu huyo akaingia chini ya matawi yaliyosongamana ya mti mkubwa, na kichwa chake kikakwama kwenye mti huo hivi kwamba akabaki amening’inia hewani huku nyumbu wake akiendelea kukimbia. 10 Mtu fulani aliona jambo hilo na kumwambia Yoabu:+ “Jamani! Nimemwona Absalomu akining’inia kwenye mti mkubwa.” 11 Yoabu akamwambia hivi mtu huyo: “Ikiwa ulimwona, kwa nini hukumuua papo hapo na kumwangusha chini? Ikiwa ungefanya hivyo, ningefurahia kukupa vipande kumi vya fedha na mshipi.” 12 Lakini mtu huyo akamwambia Yoabu: “Hata kama ningepewa vipande 1,000 vya fedha, nisingeunyoosha mkono wangu dhidi ya mwana wa mfalme, kwa maana tulimsikia mfalme akikupa agizo hili, wewe na Abishai na Itai: ‘Haidhuru wewe ni nani, mlindeni kijana Absalomu.’+ 13 Nisingetii na hivyo kumuua,* jambo hilo lingejulikana kwa mfalme siku moja, nawe hungenilinda.” 14 Ndipo Yoabu akasema: “Sitaendelea kupoteza muda pamoja nawe!” Basi akachukua mikuki mitatu midogo* na kumchoma nayo Absalomu kwenye moyo alipokuwa angali hai akining’inia kwenye mti mkubwa. 15 Kisha watumishi kumi waliombebea Yoabu silaha wakaja na kumpiga Absalomu mpaka wakamuua.+ 16 Sasa Yoabu akapiga pembe, na watu wakarudi na kuacha kuwafuatia Waisraeli; Yoabu akawaambia wasiwafuatie. 17 Wakamchukua Absalomu na kumtupa ndani ya shimo kubwa msituni, nao wakarundika rundo kubwa sana la mawe juu yake.+ Kisha Waisraeli wote wakakimbia na kurudi katika nyumba zao.

18 Absalomu alipokuwa hai, alikuwa amechukua na kujisimamishia nguzo katika Bonde la* Mfalme,+ kwa maana alisema: “Sina mwana atakayeendeleza kumbukumbu ya jina langu.”+ Basi akaiita nguzo hiyo kwa jina lake, na tangu siku hiyo inaitwa Mnara wa Ukumbusho wa Absalomu.

19 Ahimaazi+ mwana wa Sadoki akasema: “Tafadhali, niruhusu nikimbie na kumpelekea mfalme habari hizi, kwa maana Yehova amemtendea kwa haki kwa kumweka huru kutoka mikononi mwa maadui wake.”+ 20 Lakini Yoabu akamwambia: “Hutapeleka habari hizi leo. Unaweza kuzipeleka siku nyingine, lakini hutampelekea mfalme habari hizi leo kwa sababu aliyekufa ni mwana wake mwenyewe.”+ 21 Kisha Yoabu akamwambia mtu fulani Mkushi:+ “Nenda, umwambie mfalme mambo uliyoona.” Kwa hiyo Mkushi huyo akamwinamia Yoabu na kukimbia. 22 Ahimaazi mwana wa Sadoki akamwambia tena Yoabu: “Liwalo na liwe, tafadhali niruhusu nikimbie na kumfuata yule Mkushi.” Hata hivyo, Yoabu akamwambia: “Mwanangu, kwa nini ukimbie wakati huna habari yoyote ya kupeleka?” 23 Lakini bado akasema: “Liwalo na liwe, acha nikimbie.” Yoabu akamwambia: “Kimbia!” Basi Ahimaazi akakimbia kupitia njia ya wilaya ya Yordani,* na hatimaye akampita huyo Mkushi.

24 Daudi alikuwa ameketi kati ya malango mawili ya jiji,+ na mlinzi+ akapanda ukutani hadi juu ya paa la lango. Akatazama na kumwona mtu fulani akikimbia peke yake. 25 Kwa hiyo mlinzi huyo akaita kwa sauti na kumjulisha mfalme. Mfalme akasema: “Ikiwa yuko peke yake, analeta habari.” Mtu huyo alipozidi kukaribia, 26 mlinzi akamwona mtu mwingine akikimbia. Kwa hiyo mlinzi huyo akamwambia mlinda lango: “Tazama! Mtu mwingine anakimbia peke yake!” Mfalme akasema: “Huyo pia analeta habari.” 27 Mlinzi akasema: “Naona mtu wa kwanza akikimbia kama Ahimaazi+ mwana wa Sadoki,” basi mfalme akasema: “Huyo ni mtu mwema, naye analeta habari njema.” 28 Kisha Ahimaazi akamwambia hivi mfalme kwa sauti: “Mambo yote ni sawa!” Ndipo akamwinamia mfalme kifudifudi. Halafu akasema: “Abarikiwe Yehova Mungu wako, ambaye amewatia mikononi mwako wanaume waliokuasi* bwana wangu mfalme!”+

29 Hata hivyo, mfalme akauliza: “Je, kijana Absalomu hajambo?” Ahimaazi akajibu: “Niliona vurugu kubwa Yoabu alipomtuma mtumishi wa mfalme na mimi mtumishi wako, lakini sikuelewa maana yake.”+ 30 Kwa hiyo mfalme akasema: “Sogea kando, simama hapa.” Basi akasogea kando na kusimama hapo.

31 Ndipo yule Mkushi akafika+ na kusema: “Bwana wangu mfalme na apokee habari hizi: Leo Yehova ametekeleza haki kwa kukuweka huru kutoka mikononi mwa wote waliokuasi.”+ 32 Lakini mfalme akamuuliza huyo Mkushi: “Je, kijana Absalomu hajambo?” Ndipo Mkushi akajibu: “Maadui wote wa bwana wangu mfalme na wote waliokuasi ili kukudhuru na wawe kama huyo kijana!”+

33 Jambo hilo likamtaabisha mfalme, akapanda kwenye chumba kilicho paani juu ya lango na kulia, alikuwa akisema hivi huku akitembea: “Mwanangu Absalomu, mwanangu, mwanangu Absalomu! Laiti ningekufa badala yako, Absalomu mwanangu, mwanangu!”+

19 Yoabu akaletewa habari hii: “Mfalme analia na kumwombolezea Absalomu.”+ 2 Basi siku hiyo ushindi* uligeuka na kuwa maombolezo kwa watu wote, kwa sababu walisikia kwamba mfalme alikuwa akimwombolezea mwana wake. 3 Siku hiyo watu wakarudi jijini kimyakimya+ wakiona aibu kama watu waliokimbia kutoka vitani. 4 Mfalme aliufunika uso wake na kuendelea kulia kwa sauti kubwa: “Mwanangu Absalomu! Absalomu mwanangu, mwanangu!”+

5 Kisha Yoabu akaingia nyumbani kwa mfalme na kumwambia: “Leo umewaaibisha watumishi wako wote ambao siku ya leo waliokoa uhai wako,* uhai wa* wana wako,+ mabinti wako,+ wake zako, na masuria wako.+ 6 Unawapenda wale wanaokuchukia na kuwachukia wale wanaokupenda, kwa maana leo umeonyesha wazi kwamba wakuu wako na watumishi wako hawana maana kwako, kwa sababu nina hakika kwamba ikiwa Absalomu angekuwa hai leo na sisi sote tuwe tumekufa, ingekuwa sawa kwako. 7 Sasa inuka, toka nje ukawatie moyo* watumishi wako, kwa sababu naapa kwa jina la Yehova kwamba usipotoka nje, hakuna mtu atakayebaki pamoja nawe usiku wa leo. Hili litakuwa jambo baya zaidi kwako kuliko madhara yote yaliyokupata tangu ulipokuwa kijana mpaka sasa.” 8 Basi mfalme akainuka na kwenda kuketi kwenye lango la jiji, na watu wote wakaambiwa hivi: “Sasa mfalme ameketi langoni.” Kisha watu wote wakaja mbele ya mfalme.

Lakini Waisraeli walikuwa wamekimbia, kila mmoja kwenda nyumbani kwake.+ 9 Watu wote katika makabila yote ya Israeli walikuwa wakibishana, wakisema: “Mfalme alituokoa kutoka mikononi mwa maadui wetu,+ naye alituokoa kutoka mikononi mwa Wafilisti; lakini sasa ameikimbia nchi kwa sababu ya Absalomu.+ 10 Na Absalomu, tuliyemtia mafuta ili atutawale,+ amekufa vitani.+ Basi sasa, kwa nini hamfanyi lolote kumrudisha mfalme?”

11 Mfalme Daudi akatuma ujumbe huu kwa Sadoki+ na Abiathari+ waliokuwa makuhani: “Waambieni wazee wa Yuda,+ ‘Kwa nini muwe wa mwisho kunirudisha mimi mfalme nyumbani kwangu, wakati ujumbe wa Waisraeli wote umenifikia nyumbani kwangu? 12 Ninyi ni ndugu zangu; ninyi ni mfupa wangu na nyama yangu.* Kwa nini muwe wa mwisho kunirudisha mimi mfalme?’ 13 Nanyi mnapaswa kumwambia Amasa,+ ‘Je, wewe si mfupa wangu na nyama yangu? Basi Mungu na aniadhibu, tena vikali, ikiwa hutakuwa mkuu wa jeshi langu kuanzia sasa na kuendelea badala ya Yoabu.’”+

14 Kwa hiyo aliiteka* mioyo ya watu wote wa Yuda wakawa kama mtu mmoja, wakamtumia mfalme ujumbe huu: “Rudi, wewe na watumishi wako wote.”

15 Mfalme akaanza safari ya kurudi, akafika Yordani, na watu wa Yuda wakaja Gilgali+ ili kumpokea mfalme na kumsindikiza kuvuka Yordani. 16 Ndipo Shimei+ mwana wa Gera, Mbenjamini kutoka Bahurimu, akashuka haraka pamoja na watu wa Yuda ili kumpokea Mfalme Daudi, 17 naye alikuwa na wanaume 1,000 kutoka Benjamini. Pia Siba,+ mtumishi wa nyumba ya Sauli, pamoja na wanawe 15 na watumishi wake 20 wakashuka haraka kwenye Mto Yordani kabla mfalme hajafika. 18 Naye akavuka* kivuko ili kuivusha nyumba ya mfalme na kufanya lolote alilotaka. Lakini Shimei mwana wa Gera akaanguka mbele ya mfalme kifudifudi mfalme alipokuwa karibu kuvuka Mto Yordani. 19 Akamwambia mfalme: “Bwana wangu usinione kuwa na hatia, nawe usikumbuke kosa ambalo mimi mtumishi wako nilifanya+ siku ambayo bwana wangu mfalme ulitoka Yerusalemu. Mfalme, usiweke jambo hilo moyoni mwako, 20 kwa sababu mimi mtumishi wako najua vizuri kwamba nimetenda dhambi; kwa hiyo leo mimi ndiye wa kwanza kutoka katika nyumba yote ya Yosefu kushuka hapa kuja kukupokea bwana wangu mfalme.”

21 Papo hapo Abishai+ mwana wa Seruya+ akasema: “Je, Shimei hapaswi kuuawa kwa sababu hii, kwa kuwa alimtukana mtiwa-mafuta wa Yehova?”+ 22 Lakini Daudi akasema: “Jambo hili linawahusuje, ninyi wana wa Seruya,+ kwamba mtende kinyume cha matakwa yangu? Je, mtu yeyote anapaswa kuuawa leo katika Israeli? Je, sijui kwamba leo mimi ndiye mfalme wa Israeli?” 23 Kisha mfalme akamwambia Shimei: “Hutakufa.” Naye mfalme akamwapia.+

24 Mefiboshethi,+ mjukuu wa Sauli, akashuka pia kuja kumpokea mfalme. Hakuwa ameosha miguu wala kukata kucha zake wala hakuwa amenyoa masharubu yake wala kufua mavazi yake tangu siku ambayo mfalme aliondoka mpaka siku aliyorudi kwa amani. 25 Alipofika* Yerusalemu kumpokea mfalme, mfalme alimuuliza: “Mefiboshethi, kwa nini hukwenda pamoja nami?” 26 Akamjibu: “Bwana wangu mfalme, mtumishi wangu+ alinidanganya. Kwa maana mimi mtumishi wako nilikuwa nimesema, ‘Acha niweke matandiko juu ya punda wangu ili nipande juu yake na kwenda pamoja na mfalme,’ kwa maana mimi mtumishi wako ni kilema.+ 27 Lakini alinichongea kwako bwana wangu mfalme.+ Hata hivyo, wewe bwana wangu mfalme ni kama malaika wa Mungu wa kweli, basi fanya jambo lolote unaloona ni jema kwako. 28 Kwa maana wewe bwana wangu mfalme ungeiangamiza nyumba yote ya baba yangu, lakini uliniruhusu mimi mtumishi wako niwe miongoni mwa wale wanaokula mezani pako.+ Basi nina haki gani ya kuendelea kumlilia mfalme?”

29 Hata hivyo, mfalme akamwambia: “Kwa nini unaendelea kusema hivyo? Nimeamua kwamba wewe na Siba mgawane lile shamba.”+ 30 Ndipo Mefiboshethi akamwambia mfalme: “Acha achukue shamba lote, kwa sababu sasa bwana wangu mfalme umerudi kwa amani nyumbani kwako.”

31 Kisha Barzilai+ Mgileadi akashuka kutoka Rogelimu mpaka Yordani ili amsindikize mfalme hadi Yordani. 32 Barzilai alikuwa mzee sana, mwenye umri wa miaka 80, naye alimpa mfalme chakula alipokuwa akikaa Mahanaimu,+ kwa maana alikuwa tajiri sana. 33 Basi mfalme akamwambia Barzilai: “Vuka pamoja nami, nami nitakuandalia chakula huko Yerusalemu.”+ 34 Lakini Barzilai akamwambia mfalme: “Ni siku ngapi* zilizobaki za maisha yangu hivi kwamba niende nawe mfalme mpaka Yerusalemu? 35 Leo nina umri wa miaka 80.+ Je, ninaweza kutofautisha kati ya jema na baya? Je, mimi mtumishi wako ninaweza kuonja ladha ya kile ninachokula na kile ninachokunywa? Je, bado ninaweza kusikia sauti za waimbaji wa kiume na wa kike?+ Basi kwa nini mimi mtumishi wako nikuongezee mzigo bwana wangu mfalme? 36 Mimi mtumishi wako nimeridhika kukuleta wewe mfalme mpaka Yordani. Kwa nini, mfalme, unilipe thawabu hii? 37 Tafadhali, niruhusu mimi mtumishi wako nirudi, na acha nife katika jiji letu karibu na kaburi la baba yangu na mama yangu.+ Lakini mtumishi wako Kimhamu ndiye huyu.+ Acha avuke pamoja nawe bwana wangu mfalme, nawe umtendee unaloona ni jema.”

38 Basi mfalme akasema: “Kimhamu atavuka pamoja nami, nami nitamtendea ninaloona ni jema; nitakutendea wewe jambo lolote utakaloniomba.” 39 Sasa watu wote wakaanza kuvuka Yordani, na mfalme alipovuka alimbusu Barzilai+ na kumbariki; kisha Barzilai akarudi nyumbani. 40 Mfalme alipovuka kwenda Gilgali,+ Kimhamu alivuka pamoja naye. Watu wote wa Yuda na nusu ya watu wa Israeli wakamvusha mfalme.+

41 Kisha wanaume wote wa Israeli wakaja kwa mfalme na kumuuliza: “Kwa nini ndugu zetu watu wa Yuda walikuiba na kukuleta wewe mfalme na nyumba yako ng’ambo ya Yordani, pamoja na wanaume wako wote?”+ 42 Wanaume wote wa Yuda wakawajibu hivi wanaume wa Israeli: “Kwa sababu mfalme ni mtu wa jamaa yetu.+ Kwa nini jambo hili linawakasirisha? Je, tumekula chochote ambacho kimemgharimu mfalme, au je, tumepewa zawadi?”

43 Hata hivyo, wanaume wa Israeli wakawajibu hivi wanaume wa Yuda: “Tuna makabila kumi na kwa hiyo tuna haki zaidi kumhusu Mfalme Daudi kuliko ninyi. Kwa nini, basi, mmetutendea kwa dharau? Je, hatukupaswa kuwa wa kwanza kumrudisha mfalme wetu?” Lakini maneno ya wanaume wa Yuda yalikuwa makali zaidi kuliko maneno ya wanaume wa Israeli.

20 Sasa palikuwa na mfanya fujo fulani aliyeitwa Sheba,+ mwana wa Bikri, Mbenjamini. Alipiga pembe+ na kusema: “Hatuna ushirika wowote na Daudi, na hatuna urithi wowote katika mwana wa Yese.+ Enyi Waisraeli, kila mtu aende kwa miungu* yake!”+ 2 Basi wanaume wote wa Israeli wakaacha kumfuata Daudi na kuanza kumfuata Sheba mwana wa Bikri;+ lakini wanaume wa Yuda wakashikamana na mfalme wao, kuanzia Yordani mpaka Yerusalemu.+

3 Mfalme Daudi alipofika nyumbani kwake* huko Yerusalemu,+ aliwachukua wale masuria kumi aliokuwa amewaacha waitunze nyumba yake,+ akawaweka ndani ya nyumba chini ya ulinzi. Aliwapa chakula, lakini hakulala nao.+ Walibaki kifungoni mpaka siku walipokufa, nao waliishi kama wajane, ingawa mume wao alikuwa hai.

4 Sasa mfalme akamwambia Amasa:+ “Waite wanaume wa Yuda waje kwangu katika muda wa siku tatu, nawe pia unapaswa kuwepo.” 5 Kwa hiyo Amasa akaenda kuwaita wanaume wa Yuda, lakini alichelewa kurudi wakati alioambiwa arudi. 6 Ndipo Daudi akamwambia Abishai:+ “Huenda Sheba+ mwana wa Bikri atatuletea madhara makubwa zaidi kuliko Absalomu.+ Wachukue watumishi wangu mimi bwana wako umfuatie, ili asipate majiji yenye ngome na kutuponyoka.” 7 Basi wanaume wa Yoabu,+ Wakerethi, Wapelethi,+ na wanaume wote mashujaa wakaenda kumfuatia; wakaondoka Yerusalemu ili kumfuatia Sheba mwana wa Bikri. 8 Walipokaribia jiwe kubwa lililoko Gibeoni,+ Amasa+ akaja kuwapokea. Sasa Yoabu alikuwa amevaa mavazi yake ya vita, naye alikuwa ametia upanga katika ala yake na kuufungia kiunoni. Aliposogea mbele, upanga huo ukaanguka.

9 Yoabu akamuuliza Amasa: “Je, hali yako ni njema ndugu yangu?” Kisha Yoabu akamshika Amasa ndevu kwa mkono wa kulia kana kwamba anataka kumbusu. 10 Amasa hakuchukua tahadhari kuhusiana na upanga uliokuwa mkononi mwa Yoabu, basi Yoabu akamchoma tumboni kwa upanga huo,+ na matumbo yake yakamwagika ardhini. Hakuhitaji kumchoma tena; alikufa alipochomwa mara moja. Kisha Yoabu na ndugu yake Abishai wakamfuatia Sheba mwana wa Bikri.

11 Mmoja wa vijana wa Yoabu akasimama karibu na Amasa na kusema: “Yeyote anayemuunga mkono Yoabu na yeyote ambaye ni wa Daudi, na amfuate Yoabu!” 12 Wakati huo wote Amasa alikuwa akigaagaa kwenye damu yake katikati ya barabara. Kijana huyo alipoona kwamba watu wote walikuwa wakisimama hapo, akamwondoa Amasa barabarani na kumpeleka shambani. Kisha akatupa vazi juu yake, kwa sababu aliona kwamba kila mtu aliyefika mahali alipokuwa alisimama. 13 Baada ya kumwondoa barabarani, wanaume wote walimfuata Yoabu ili kumfuatia Sheba+ mwana wa Bikri.

14 Sheba akapita miongoni mwa makabila yote ya Israeli mpaka jiji la Abeli la Beth-maaka.+ Wabikri wakakusanyika pamoja na kumfuata.

15 Yoabu na wanaume wake wakaja na kumzingira katika jiji la Abeli la Beth-maaka na kutengeneza boma kuzunguka jiji hilo, kwani lilikuwa ndani ya boma. Na wanaume wote waliokuwa pamoja na Yoabu walikuwa wakiuharibu ukuta ili kuuangusha chini. 16 Na mwanamke fulani mwenye hekima akasema hivi kwa sauti kutoka jijini: “Sikilizeni wanaume, sikilizeni! Tafadhali, mwambieni Yoabu aje hapa, ili niongee naye.” 17 Basi Yoabu akamkaribia, kisha mwanamke huyo akamuuliza: “Je, wewe ni Yoabu?” Akamjibu: “Ndiyo.” Ndipo mwanamke huyo akamwambia: “Yasikilize maneno yangu mimi kijakazi wako.” Yoabu akasema: “Ninasikiliza.” 18 Mwanamke huyo akaendelea kusema: “Zamani walikuwa wakisema, ‘Acheni watafute ushauri kule Abeli, na hivyo ndivyo walivyotatua matatizo.’ 19 Mimi ni mmojawapo wa watu wanaopenda amani na waaminifu katika Israeli. Unataka kuliharibu jiji ambalo ni kama mama katika Israeli. Kwa nini uangamize* urithi wa Yehova?”+ 20 Yoabu akamjibu hivi: “Ni jambo nisiloweza kamwe kuwazia kwamba niliangamize na kuliharibu. 21 Sivyo ilivyo. Lakini mtu fulani anayeitwa Sheba+ mwana wa Bikri kutoka eneo lenye milima la Efraimu+ amemwasi* Mfalme Daudi. Mkimtoa nje mtu huyo, nitaondoka jijini.” Ndipo mwanamke huyo akamwambia Yoabu: “Haya! Utatupiwa kichwa chake ukutani!”

22 Mara moja mwanamke huyo mwenye hekima akaenda kuzungumza na watu wote, nao wakamkata kichwa Sheba mwana wa Bikri na kukitupa kwa Yoabu. Basi Yoabu akapiga pembe, nao wakatawanyika kutoka kwenye jiji hilo, kila mmoja akarudi nyumbani kwake;+ naye Yoabu akarudi Yerusalemu kwa mfalme.

23 Yoabu alikuwa mkuu wa jeshi lote la Israeli;+ Benaya+ mwana wa Yehoyada+ alikuwa mkuu wa Wakerethi na Wapelethi.+ 24 Adoramu+ alikuwa msimamizi wa wale walioandikishwa kufanya kazi ya kulazimishwa; na Yehoshafati+ mwana wa Ahiludi alifanya kazi ya kuweka kumbukumbu. 25 Sheva alikuwa mwandishi; Sadoki+ na Abiathari+ walikuwa makuhani. 26 Na Ira, Myairi, akawa pia mhudumu mkuu* wa Daudi.

21 Basi katika siku za Daudi kulikuwa na njaa kali+ kwa miaka mitatu mfululizo, kwa hiyo Daudi akamwomba Yehova ushauri, kisha Yehova akasema: “Sauli na nyumba yake wana hatia ya damu, kwa sababu aliwaua Wagibeoni.”+ 2 Basi mfalme akawaita Wagibeoni+ na kuongea nao. (Sasa, Wagibeoni hawakuwa Waisraeli bali walikuwa Waamori+ waliokuwa wamebaki, na Waisraeli walikuwa wameapa kwamba hawatawaua,+ lakini Sauli akichochewa na bidii yake kwa ajili ya watu wa Israeli na Yuda alitaka kuwaangamiza.) 3 Daudi akawauliza Wagibeoni: “Niwafanyie nini, nami nitawalipaje kwa ajili ya mliyotendewa, ili muubariki urithi wa Yehova?” 4 Wagibeoni wakamwambia: “Jambo ambalo Sauli na nyumba yake walitutendea si suala la fedha wala dhahabu;+ wala hatuwezi kumuua mtu yeyote katika Israeli.” Daudi akasema: “Nitawafanyia jambo lolote mtakalosema.” 5 Wakamwambia mfalme: “Mtu aliyetuua na kupanga njama ya kutuangamiza ili tusiishi katika eneo lolote la Israeli+— 6 tupatieni wanawe saba. Tutatundika maiti zao*+ mbele za Yehova katika jiji la Gibea+ la Sauli, aliyechaguliwa na Yehova.”+ Ndipo mfalme akasema: “Nitawapa.”

7 Hata hivyo, mfalme akamhurumia Mefiboshethi,+ mwana wa Yonathani mwana wa Sauli, kwa sababu ya kiapo ambacho Daudi na Yonathani mwana wa Sauli walikuwa wameapiana mbele za Yehova.+ 8 Basi mfalme akamchukua Armoni na Mefiboshethi, wana wawili ambao Rispa+ binti ya Aya alimzalia Sauli, na wana watano ambao Mikali*+ binti ya Sauli alimzalia Adrieli+ mwana wa Barzilai, Mmeholathi. 9 Daudi akawapa Wagibeoni wana hao, nao wakatundika maiti zao mlimani mbele za Yehova.+ Wana wote saba walikufa pamoja; waliuawa siku za kwanza za mavuno, mwanzoni mwa mavuno ya shayiri. 10 Kisha Rispa+ binti ya Aya akachukua gunia na kulitandika mwambani tangu mwanzo wa mavuno mpaka mvua kutoka mbinguni iliponyeshea maiti hizo; hakuruhusu ndege wa angani watue juu ya maiti hizo wakati wa mchana wala wanyama wa mwituni wazikaribie wakati wa usiku.

11 Daudi akaambiwa mambo ambayo Rispa binti ya Aya suria wa Sauli alikuwa amefanya. 12 Kwa hiyo Daudi akaenda na kuchukua mifupa ya Sauli na mifupa ya Yonathani mwana wake kutoka kwa viongozi* wa Yabesh-gileadi,+ waliokuwa wameiba mifupa hiyo katika uwanja wa jiji la Beth-shani, ambako Wafilisti walikuwa wamewatundika siku ambayo walimuua Sauli juu ya Gilboa.+ 13 Akachukua mifupa ya Sauli na mifupa ya Yonathani mwana wake kutoka mlimani, pia wakaikusanya mifupa ya wanaume waliokuwa wameuawa.*+ 14 Kisha wakaizika mifupa ya Sauli na Yonathani mwana wake katika nchi ya Benjamini kule Sela+ katika kaburi la Kishi+ baba yake. Baada ya kufanya kila jambo ambalo mfalme alikuwa ameamuru, Mungu akasikiliza maombi yao ya kumsihi kuhusu nchi.+

15 Vita vikatokea tena kati ya Wafilisti na Waisraeli.+ Kwa hiyo, Daudi na watumishi wake wakashuka kwenda kupigana na Wafilisti, lakini Daudi akachoka. 16 Mzao wa Warefaimu+ aliyeitwa Ishbi-benobu, aliyekuwa na mkuki wa shaba wenye uzito wa shekeli 300*+ na aliyejihami kwa upanga mpya, alikusudia kumuua Daudi. 17 Mara moja Abishai+ mwana wa Seruya akaja kumsaidia,+ akampiga Mfilisti huyo na kumuua. Wakati huo wanaume wa Daudi wakamwapia hivi: “Usiende tena vitani pamoja nasi!+ Usiizime taa ya Israeli!”+

18 Baada ya hayo, wakapigana tena na Wafilisti+ kule Gobu. Wakati huo Sibekai+ Mhusha alimuua Safu, aliyekuwa mzao wa Warefaimu.+

19 Wakapigana tena na Wafilisti+ huko Gobu, na Elhanani mwana wa Yaare-oregimu Mbethlehemu akamuua Goliathi Mgathi, aliyekuwa na mkuki wenye mpini kama mti wa wafumaji wa nguo.+

20 Vita vikatokea tena huko Gathi, ambako kulikuwa na mwanamume mkubwa isivyo kawaida, mwenye vidole 6 katika kila mkono na vidole 6 katika kila mguu, jumla ya vidole 24; naye pia alikuwa mzao wa Warefaimu.+ 21 Aliendelea kuwadhihaki Waisraeli.+ Basi Yonathani mwana wa Shimei,+ ndugu ya Daudi, akamuua.

22 Watu hao wanne walikuwa wazao wa Warefaimu huko Gathi, na Daudi na watumishi wake ndio waliowaua.+

22 Daudi akamwimbia Yehova maneno ya wimbo huu+ siku ambayo Yehova alimwokoa kutoka mikononi mwa maadui wake wote+ na kutoka mikononi mwa Sauli.+ 2 Akasema:

“Yehova ni jabali langu na ngome yangu+ na Mwokozi wangu.+

 3 Mungu wangu ni mwamba wangu,+ ninayemkimbilia,

Ngao yangu+ na pembe* yangu ya wokovu,* kimbilio langu salama*+

Na mahali pangu pa kukimbilia,+ mwokozi wangu;+ wewe unayeniokoa kutoka katika ukatili.

 4 Ninamlilia Yehova, anayestahili kusifiwa,

Nami nitaokolewa kutoka kwa maadui wangu.

 5 Mawimbi ya kifo yalinizunguka pande zote;+

Mafuriko ya ghafla ya wanaume wasiofaa kitu yaliniogopesha.+

 6 Kamba za Kaburi* zilinizunguka;+

Mitego ya kifo ilinikabili.+

 7 Katika taabu yangu nilimwita Yehova,+

Niliendelea kumlilia Mungu wangu.

Kisha akiwa katika hekalu lake akaisikia sauti yangu,

Na kilio changu cha kuomba msaada kilifika masikioni mwake.+

 8 Dunia ikaanza kutetemeka na kutikisika huku na huku;+

Misingi ya mbingu ikasukasuka+

Nayo ikatikisika huku na huku kwa sababu alikuwa amekasirishwa.+

 9 Moshi ulipanda kutoka katika mianzi ya pua yake,

Na moto unaoteketeza kabisa ukatoka kinywani mwake;+

Makaa ya mawe yanayowaka moto mkali yakatoka kwake.

10 Alizifanya mbingu zijikunje alipokuwa akishuka,+

Na giza zito lilikuwa chini ya miguu yake.+

11 Alipanda juu ya kerubi,+ akaja akiruka.

Alionekana juu ya mabawa ya kiumbe wa roho.*+

12 Kisha akaweka giza kumzunguka kama kibanda,+

Katika maji yenye giza na mawingu mazito.

13 Kutoka katika mwangaza ulio mbele zake makaa ya mawe yenye moto mkali yaliwaka.

14 Kisha Yehova akaanza kunguruma kutoka mbinguni;+

Aliye Juu Zaidi aliifanya sauti yake isikike.+

15 Alipiga mishale yake+ akawatawanya;

Radi, akawavuruga.+

16 Sakafu ya bahari ikaonekana;+

Misingi ya nchi ikafunuliwa kwa kemeo la Yehova,

Kwa mlipuko wa pumzi kutoka katika mianzi ya pua yake.+

17 Aliunyoosha mkono wake kutoka juu;

Akanishika na kunivuta kutoka katika maji yenye kina.+

18 Aliniokoa kutoka kwa adui yangu mwenye nguvu,+

Kutoka kwa wale wanaonichukia, waliokuwa na nguvu nyingi kuliko mimi.

19 Walinikabili katika siku ya msiba wangu,+

Lakini Yehova alikuwa tegemeo langu.

20 Alinitoa nje na kunileta mahali penye usalama;*+

Aliniokoa kwa sababu alipendezwa nami.+

21 Yehova hunithawabisha kulingana na uadilifu wangu;+

Hunilipa kulingana na usafi wa* mikono yangu.+

22 Kwa maana nimezishika njia za Yehova,

Nami sijamwacha kwa uovu Mungu wangu.

23 Hukumu zake zote+ ziko mbele yangu;

Sitageuka kando kutoka kwenye sheria zake.+

24 Nitabaki bila lawama+ mbele zake,

Nami nitajiepusha na uovu.+

25 Yehova na anilipe kulingana na uadilifu wangu,+

Kulingana na usafi wangu* mbele zake.+

26 Kwa mtu mshikamanifu unatenda kwa ushikamanifu;+

Kwa mtu asiye na lawama, mtu hodari, unatenda bila lawama;+

27 Kwa walio safi unajidhihirisha mwenyewe kuwa safi,+

Lakini kwa waliopotoka unajidhihirisha mwenyewe kuwa mwenye busara.*+

28 Kwa maana wewe huwaokoa walio wanyenyekevu,+

Lakini macho yako hayapendezwi na wenye kiburi, nawe huwashusha.+

29 Kwa maana wewe ni taa yangu, Ee Yehova;+

Yehova ndiye anayefanya giza langu liangaze.+

30 Kwa msaada wako ninaweza kukabiliana na kundi la wavamizi;

Kwa nguvu za Mungu ninaweza kuupanda ukuta.+

31 Njia ya Mungu wa kweli ni kamilifu;+

Neno la Yehova ni safi.+

Yeye ni ngao kwa wote wanaomkimbilia.+

32 Kwa maana ni nani aliye Mungu ila Yehova?+

Na ni nani aliye mwamba isipokuwa Mungu wetu?+

33 Mungu wa kweli ni ngome yangu imara,+

Naye ataifanya njia yangu iwe kamilifu.+

34 Huifanya miguu yangu iwe kama ya paa;

Hunifanya nisimame mahali palipo juu.+

35 Huizoeza mikono yangu kupigana vita;

Mikono yangu inaweza kuukunja upinde wa shaba.

36 Wewe hunipa ngao yako ya wokovu,

Na unyenyekevu wako hunifanya niwe mkuu.+

37 Unapanua njia kwa ajili ya hatua zangu;

Miguu yangu haitateleza.*+

38 Nitawafuatia maadui wangu na kuwaangamiza;

Sitarudi mpaka watakapoangamizwa kabisa.

39 Nami nitawaangamiza kabisa na kuwaponda, hivi kwamba hawatainuka;+

Wataanguka chini ya miguu yangu.

40 Utanipa nguvu kwa ajili ya vita;+

Utawafanya maadui wangu waanguke chini yangu.+

41 Utawafanya maadui wangu wanikimbie;*+

Nitawakomesha* wale wanaonichukia.+

42 Wanalilia msaada, lakini

hakuna mtu wa kuwaokoa;

Hata wanamlilia Yehova, lakini yeye hawajibu.+

43 Nitawaponda wawe laini kama mavumbi ya dunia;

Nitawapondaponda na kuwakanyaga-kanyaga kama matope barabarani.

44 Utaniokoa kutoka kwa watu wangu ambao hutafuta makosa.+

Utanilinda niwe kiongozi wa mataifa;+

Watu ambao siwajui watanitumikia.+

45 Wageni watakuja wakijikunyata mbele zangu;+

Watanitii kwa sababu ya mambo watakayosikia kunihusu.*

46 Wageni watakosa ujasiri;*

Watakuja wakitetemeka kutoka katika ngome zao.

47 Yehova yuko hai! Mwamba wangu na asifiwe!+

Mungu wa mwamba wa wokovu wangu na akwezwe.+

48 Mungu wa kweli hunilipizia kisasi;+

Huyatiisha mataifa chini yangu;+

49 Yeye huniokoa kutoka kwa maadui wangu.

Unaniinua juu+ ya wale wanaonishambulia;

Unaniokoa kutoka kwa mtu mkatili.+

50 Ndiyo sababu nitakushukuru wewe, Ee Yehova, miongoni mwa mataifa,+

Nami nitaliimbia sifa* jina lako:+

51 Yeye hutenda matendo makuu ya wokovu kwa ajili ya mfalme wake;*+

Humtendea mtiwa-mafuta wake kwa upendo mshikamanifu,

Kwa Daudi na kwa uzao wake* milele.”+

23 Haya ndiyo maneno ya mwisho ya Daudi:+

“Neno la Daudi mwana wa Yese,+

Na neno la mwanamume aliyeinuliwa juu,+

Mtiwa-mafuta+ wa Mungu wa Yakobo,

Mwimbaji anayependeza* wa nyimbo+ za Israeli.

 2 Roho ya Yehova ilisema kupitia mimi;+

Neno lake lilikuwa kwenye ulimi wangu.+

 3 Mungu wa Israeli alisema;

Mwamba wa Israeli+ aliniambia:

‘Yule anayetawala wanadamu anapokuwa mwadilifu,+

Anapotawala kwa kumwogopa Mungu,+

 4 Ni kama mwangaza wa asubuhi jua linapoangaza,+

Asubuhi isiyo na mawingu.

Ni kama mwangaza baada ya mvua kunyesha,

Ambao unaotesha majani duniani.’+

 5 Je, sivyo ilivyo nyumba yangu mbele za Mungu?

Kwa maana amefanya pamoja nami agano la milele,+

Lililopangwa kwa utaratibu katika kila jambo na kuhakikishwa.

Kwa sababu linamaanisha wokovu wangu wote na furaha yangu yote,

Je, yeye halifanyi lisitawi kwa sababu hiyo?+

 6 Lakini watu wasiofaa kitu hutupwa+ wote kama vichaka vya miiba,

Kwa maana hawawezi kuchukuliwa kwa mkono.

 7 Mtu anapowagusa,

Anapaswa kujihami kikamili kwa chuma na mpini wa mkuki,

Nao wanapaswa kuteketezwa kabisa kwa moto mahali walipo.”

8 Haya ndiyo majina ya mashujaa hodari wa Daudi:+ Yosheb-bashebethi Mtakemoni, kiongozi wa wale watatu.+ Wakati mmoja, alitumia mkuki wake kuwaua watu 800. 9 Aliyemfuata ni Eleazari+ mwana wa Dodo+ mwana wa Ahohi, naye alikuwa miongoni mwa mashujaa hao watatu hodari waliokuwa na Daudi walipowadhihaki Wafilisti. Walikuwa wamekusanyika huko kwa ajili ya vita, na wanaume wa Israeli walipokimbia, 10 alisimama imara na kuendelea kuwaua Wafilisti mpaka mkono wake ulipochoka na kuganda kwa sababu ya kuushika upanga.+ Basi Yehova akawapa ushindi* mkubwa siku hiyo;+ na watu wakamfuata Eleazari ili kuchukua nyara za watu waliouawa.

11 Aliyemfuata ni Shamma mwana wa Agee, Mharari. Wafilisti walikusanyika kule Lehi, mahali ambapo palikuwa na shamba lililojaa dengu; na watu wakakimbia kwa sababu ya Wafilisti. 12 Lakini alisimama katikati ya shamba hilo na kuwazuia Wafilisti wasiingie humo, naye aliendelea kuwaua Wafilisti, hivi kwamba Yehova akawapa ushindi* mkubwa.+

13 Viongozi watatu kati ya wale viongozi 30 walishuka wakati wa mavuno kwenda kwa Daudi katika pango la Adulamu,+ na kikosi* cha Wafilisti kilikuwa kimepiga kambi katika Bonde la* Refaimu.+ 14 Wakati huo Daudi alikuwa ndani ya ngome,+ na kituo cha ulinzi cha Wafilisti kilikuwa Bethlehemu. 15 Kisha Daudi akasema alichotamani: “Laiti ningekunywa maji kutoka katika tangi lililo karibu na lango la Bethlehemu!” 16 Ndipo wale mashujaa watatu hodari wakaingia kwa nguvu katika kambi ya Wafilisti, wakateka maji kutoka katika tangi hilo lililo karibu na lango la Bethlehemu na kumletea Daudi; lakini akakataa kuyanywa, akayamwaga mbele za Yehova.+ 17 Akasema: “Ni jambo nisiloweza kamwe kuwazia, Ee Yehova, kufanya hivyo! Je, ninywe damu+ ya wanaume walioenda kuhatarisha uhai wao?”* Basi akakataa kuyanywa. Hayo ndiyo mambo waliyotenda mashujaa wake watatu hodari.

18 Abishai+ ndugu ya Yoabu mwana wa Seruya+ alikuwa kiongozi wa wengine watatu; alitumia mkuki wake kuwaua watu 300, naye alikuwa maarufu kama wale watatu.+ 19 Ingawa alikuwa mashuhuri zaidi kuliko wale wengine watatu na alikuwa kiongozi wao, hakuwa shujaa kama wale watatu wa kwanza.

20 Benaya+ mwana wa Yehoyada alikuwa mwanamume jasiri* aliyefanya mambo mengi ya kishujaa kule Kabzeeli.+ Aliwaua wana wawili wa Arieli wa Moabu, naye aliingia ndani ya shimo la maji siku ya theluji na kumuua simba.+ 21 Alimuua pia mwanamume Mmisri aliyekuwa mkubwa isivyo kawaida. Ingawa Mmisri huyo alikuwa na mkuki mkononi, Benaya alikabiliana naye akiwa na fimbo, akamnyang’anya Mmisri huyo mkuki kutoka mkononi mwake na kumuua kwa mkuki wake mwenyewe. 22 Benaya mwana wa Yehoyada alifanya mambo hayo, naye alikuwa maarufu kama wale mashujaa watatu hodari. 23 Ingawa alikuwa mashuhuri hata kuliko wale 30, hakuwa shujaa kama wale watatu. Lakini Daudi alimweka kuwa kiongozi wa walinzi wake binafsi.

24 Asaheli+ ndugu ya Yoabu alikuwa miongoni mwa wale 30: Elhanani mwana wa Dodo wa Bethlehemu,+ 25 Shamma Mharodi, Elika Mharodi, 26 Helezi+ Mpeleti, Ira+ mwana wa Ikeshi Mtekoa, 27 Abiezeri+ Mwanathothi,+ Mebunai Mhusha, 28 Salmoni Mwahohi, Maharai+ Mnetofa, 29 Helebu mwana wa Baana Mnetofa, Itai mwana wa Ribai wa jiji la Gibea la Wabenjamini, 30 Benaya+ Mpirathoni, Hidai kutoka katika makorongo* ya Gaashi,+ 31 Abi-alboni Mwarbathi, Azmavethi Mbarhumu, 32 Eliaba Mshaalboni, wana wa Yasheni, Yonathani,⁠ 33 Shamma Mharari, Ahiamu, mwana wa Sharari Mharari, 34 Elifeleti mwana wa Ahasbai mwana wa yule Mmaakathi, Eliamu mwana wa Ahithofeli+ Mgiloni, 35 Hezro Mkarmeli, Paarai Mwarabi, 36 Igali mwana wa Nathani wa Soba, Bani Mgadi, 37 Seleki Mwamoni, Naharai Mbeerothi, aliyembebea silaha Yoabu mwana wa Seruya, 38 Ira Mwithri, Garebu Mwithri,+ 39 na Uria+ Mhiti—wote walikuwa 37.

24 Hasira ya Yehova ikawaka tena dhidi ya Waisraeli+ mtu fulani alipomchochea Daudi* atende kinyume chao kwa kumwambia: “Nenda, ukawahesabu+ watu wa Israeli na Yuda.”+ 2 Basi mfalme akamwambia Yoabu+ mkuu wa jeshi aliyekuwa pamoja naye: “Tafadhali nenda katika makabila yote ya Israeli, kuanzia Dani mpaka Beer-sheba,+ uwaandikishe watu, ili nijue idadi yao.” 3 Lakini Yoabu akamwambia mfalme: “Yehova Mungu wako na azidishe idadi ya watu mara 100, na macho yako bwana wangu mfalme na yaone jambo hilo, lakini kwa nini bwana wangu mfalme unataka kufanya jambo la namna hii?”

4 Lakini neno la mfalme likawa na nguvu kuliko neno la Yoabu na wakuu wa jeshi. Basi Yoabu na wakuu wa jeshi wakaondoka mbele ya mfalme na kwenda kuwaandikisha watu wa Israeli.+ 5 Wakavuka Yordani na kupiga kambi Aroeri,+ upande wa kulia* wa jiji katikati ya bonde, kuelekea kwa Wagadi, na mpaka Yazeri.+ 6 Kisha wakaenda mpaka Gileadi+ na nchi ya Tahtim-hodshi, wakaendelea mpaka Dani-yaani nao wakazunguka mpaka Sidoni.+ 7 Kisha wakaenda kwenye ngome ya Tiro+ na katika majiji yote ya Wahivi+ na ya Wakanaani, mwishowe wakafika Negebu+ ya Yuda kule Beer-sheba.+ 8 Kwa hiyo wakapita katika nchi yote na kurudi Yerusalemu baada ya miezi tisa na siku 20. 9 Basi Yoabu akampa mfalme idadi ya watu walioandikishwa. Mashujaa wa Israeli waliojihami kwa mapanga walikuwa 800,000, na wanaume wa Yuda walikuwa 500,000.+

10 Lakini moyo wa Daudi ukajaa* majuto+ baada ya kuwahesabu watu. Basi Daudi akamwambia Yehova: “Nimetenda dhambi+ kubwa kwa kufanya jambo hili. Na sasa, Yehova, tafadhali nisamehe kosa langu mimi mtumishi wako,+ kwa maana nimetenda kwa upumbavu sana.”+ 11 Daudi alipoamka asubuhi, neno la Yehova likamjia nabii Gadi,+ mwonaji wa Daudi, likisema: 12 “Nenda ukamwambie Daudi, ‘Yehova anasema hivi: “Ninakupa mambo matatu ya kuchagua. Chagua jambo nitakalokutendea.”’”+ 13 Basi Gadi akaenda kwa Daudi na kumwambia: “Je, unataka njaa kali ije katika nchi yako kwa miaka saba?+ Au unataka kuwakimbia maadui wako kwa miezi mitatu huku wakikufuatia? + Au unataka nchi yako ikumbwe na ugonjwa hatari kwa siku tatu?+ Sasa fikiria kwa makini jibu ninalopaswa kumpa Yule aliyenituma.” 14 Kwa hiyo Daudi akamwambia Gadi: “Jambo hilo linanihuzunisha sana. Tafadhali, acha tuanguke mkononi mwa Yehova,+ kwa maana rehema zake ni nyingi;+ lakini usiniache nianguke mkononi mwa mwanadamu.”+

15 Ndipo Yehova akaleta ugonjwa hatari+ Israeli kuanzia asubuhi mpaka wakati uliowekwa, hivi kwamba watu 70,000 wakafa+ kuanzia Dani mpaka Beer-sheba.+ 16 Malaika alipounyoosha mkono wake kuelekea jiji la Yerusalemu ili kuliangamiza, Yehova akaghairi* kwa sababu ya msiba huo,+ akamwambia malaika aliyekuwa akiwaangamiza watu: “Imetosha! Sasa shusha mkono wako.” Malaika wa Yehova alikuwa karibu na uwanja wa kupuria nafaka wa Arauna+ Myebusi.+

17 Daudi alipomwona malaika aliyekuwa akiwaangamiza watu, akamwambia Yehova: “Mimi ndiye niliyetenda dhambi, na mimi ndiye niliyekosea; lakini kondoo hawa+—wamefanya nini? Tafadhali, acha mkono wako uniadhibu mimi na nyumba ya baba yangu.”+

18 Basi Gadi akaenda kwa Daudi siku hiyo na kumwambia: “Panda ukamjengee Yehova madhabahu kwenye uwanja wa kupuria nafaka wa Arauna Myebusi.”+ 19 Basi Daudi akapanda kulingana na neno la Gadi, kama Yehova alivyoamuru. 20 Arauna alipotazama chini na kumwona mfalme na watumishi wake wakija kumwelekea, mara moja Arauna akatoka nje na kumwinamia mfalme kifudifudi. 21 Arauna akamuuliza: “Bwana wangu mfalme kwa nini umekuja kwangu mimi mtumishi wako?” Daudi akamjibu: “Kununua uwanja wako wa kupuria ili nimjengee Yehova madhabahu, ili ugonjwa hatari ambao umewakumba watu ukomeshwe.”+ 22 Lakini Arauna akamwambia Daudi: “Bwana wangu mfalme uchukue na kutoa unachoona ni chema.* Ndio hawa ng’ombe kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa na kifaa cha kupuria nafaka na nira za ng’ombe utakazotumia kama kuni. 23 Ee mfalme, mimi Arauna nimekupa vitu hivi vyote.” Kisha Arauna akamwambia mfalme: “Yehova Mungu wako na akupe kibali.”

24 Hata hivyo, mfalme akamwambia Arauna: “Hapana, ni lazima niununue kwa bei fulani. Sitamtolea Yehova Mungu wangu dhabihu za kuteketezwa ambazo hazinigharimu chochote.” Basi Daudi akanunua uwanja huo wa kupuria nafaka na hao ng’ombe kwa shekeli 50 za fedha.*+ 25 Kisha Daudi akamjengea Yehova madhabahu+ mahali hapo na kutoa dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ushirika. Ndipo Yehova akakubali maombi ya kusihi yaliyotolewa kwa ajili ya nchi,+ na ugonjwa hatari uliowakumba Waisraeli ukakomeshwa.

Au “kuwaua.”

Au “kupendeza.”

Au “kushindana.”

Tnn., “alikuwa na miguu myepesi.”

Tnn., “kunyafua.”

Au labda, “kupitia eneo lote la Bithroni.”

Tnn., “na tazama! mkono wangu uko pamoja nawe ili.”

Au “ambacho nafsi yako inatamani.”

Tnn., “kwa sababu ya damu ya.”

Huenda maneno hayo yanarejelea mwanamume mlemavu aliyelazimika kufanya kazi ya wanawake.

Tnn., “kwa shaba.”

Tnn., “wana wa ukosefu wa uadilifu.”

Au “mkate wa maombolezo.”

Yaani, watu wote wa Daudi.

Tnn., “mikono yake ikalegea.”

Au “kiwete.”

Au “aliyeikomboa nafsi yangu.”

Tnn., “Tuna uhusiano wa damu nawe.”

Tnn., “uliyekuwa ukiwatoa nje na kuwaingiza ndani Waisraeli.”

Au “wanaoichukia nafsi ya Daudi.”

Au labda, “naye akaiita.”

Au “Milo.” Neno la Kiebrania linalomaanisha “jaza.”

Au “jumba la mfalme.”

Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”

Maana yake “Bwana Anayepasua na Kupita.”

Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”

Au labda, “katikati ya.”

Maana yake “Ghadhabu Dhidi ya Uza.”

Tnn., “amejifunga.”

Au “jumba lake mwenyewe la mfalme.”

Tnn., “nikitembea.”

Tnn., “wana wote wa Israeli.”

Au “ukoo wa kifalme.”

Tnn., “mbegu yako.”

Tnn., “yule atakayetoka katika viungo vyako vya ndani.”

Au labda, “Adamu.”

Au “na hii ni sheria.”

Au “kulingana na mapenzi yako.”

Au “ukoo wa kifalme.”

Tnn., “nimepata moyo wa.”

Au “wokovu.”

Au “wokovu.”

Tnn., “walikuwa makuhani.”

Au “ni kiwete.”

Tnn., “mkate.”

Tnn., “umegeuza uso wako kuelekea.”

Au labda, “meza yangu.”

Tnn., “wanaume wa Tobu.”

Tnn., “wanaume wa Tobu.”

Tnn., “mikononi mwa.”

Yaani, majira ya kuchipua.

Au “jumba la mfalme.”

Huenda ni uchafu wa hedhi.

Tnn., “ukanawe miguu yako.”

Au “fungu la mfalme,” yaani, fungu ambalo mwenyeji humtumia mgeni mheshimiwa.

Au “kama nafsi yako inavyoishi.”

Tnn., “lilikuwa jambo ovu machoni pa.”

Au “juani.”

Au “juani.”

Au “amefutilia mbali dhambi yako.”

Au “katika jumba lake la mfalme.”

Jina hilo linatokana na neno la Kiebrania linalomaanisha “Amani.”

Maana yake “Mpendwa wa Yah.”

Au “jiji la ufalme huo.”

Huenda maneno haya yanarejelea vyanzo vya maji vya jiji hilo.

Tnn., “nalo litaitwa kwa jina langu.”

Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.

Au “mkate wa faraja.”

Au “mkate wa faraja.”

Au “Niletee mkate wa faraja.”

Au “lenye mapambo.”

Au “amepata faraja.”

Tnn., “akayatia maneno hayo kinywani mwake.”

Au “nafsi ya.”

Yaani, tumaini la mwisho la kupata wazao.

Tnn., “baki.”

Au “nafsi.”

Tnn., “kutia maneno hayo yote katika kinywa changu.”

Karibu kilogramu 2.3. Angalia Nyongeza B14.

Huenda ilikuwa mizani yenye kipimo hususa iliyotumiwa katika jumba la mfalme au shekeli ya “kifalme” iliyokuwa tofauti na shekeli ya kawaida.

Au labda, “miaka 40.”

Au “nitamwabudu; nitamtumikia.”

Au “jumba la mfalme.”

Au “waliovuka upande wake.”

Au “wakavuka mbele ya uso wa mfalme.”

Au “msiri wa.”

Hasa tini na labda pia tende.

Au “nafsi yangu.”

Tnn., “wakajiburudisha.”

Au “msiri wa.”

Au “walitunze jumba la mfalme.”

Au “ulionwa kama ushauri uliotafutwa kutoka kwa.”

Au “amedhoofika mikono yote miwili.”

Au “na wana uchungu nafsini.”

Au “mashimo; mabonde.”

Au “amekusudia.”

Tnn., “mtamezwa.”

Au “akajinyonga.”

Tnn., “mkono wa.”

Tnn., “hawataweka moyo wao juu yetu.”

Tnn., “uliwala.”

Au “Ikiwa ningeitendea nafsi yake kwa hila.”

Au labda, “vishale.” Tnn., “fito za chuma.”

Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”

Tnn., “ile wilaya.”

Tnn., “walioinua mkono wao dhidi yako.”

Au “wokovu.”

Au “nafsi yako.”

Au “nafsi ya.”

Tnn., “ukazungumze na moyo wa.”

Tnn., “nina uhusiano wa damu nanyi.”

Tnn., “aliikunja.”

Au labda, “Nao wakavuka.”

Au labda, “Alipotoka.”

Tnn., “Ni siku ngapi za miaka.”

Au labda, “katika mahema.”

Au “katika jumba lake la mfalme.”

Tnn., “uumeze.”

Tnn., “ameuinua mkono wake dhidi ya.”

Tnn., “akawa pia kuhani.”

Tnn., “tutawaanika,” yaani, mikono na miguu yao ikiwa imevunjwa.

Au labda, “Merabu.”

Au labda, “wamiliki wa mashamba.”

Tnn., “wameanikwa.”

Karibu kilogramu 3.42. Angalia Nyongeza B14.

Angalia Kamusi.

Au “mwokozi wangu mwenye nguvu.”

Au “kilele changu salama.”

Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.

Au “ya upepo.”

Au “mahali penye nafasi kubwa.”

Au “ukosefu wa hatia wa.”

Au “ukosefu wangu wa hatia.”

Au labda, “unatenda kama mpumbavu.”

Au “Vifundo vya miguu yangu havitateleza.”

Au “Utanionyesha migongo ya maadui wangu.”

Au “Nitawanyamazisha.”

Tnn., “Mara tu sikio lao linaposikia, watanitii.”

Au “watafifia.”

Au “nitalipigia muziki.”

Au “humpa ushindi mkubwa mfalme wake.”

Tnn., “mbegu yake.”

Tnn., “Yule anayependeza.”

Au “wokovu.”

Au “wokovu.”

Au “kijiji cha mahema.”

Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”

Au “nafsi zao.”

Tnn., “mwana wa mwanamume jasiri.”

Angalia Kamusi.

Au “Daudi alipochochewa.”

Au “kusini.”

Au “dhamiri ya Daudi ikajaa.”

Au “akahuzunika.”

Tnn., “kilicho chema machoni pako.”

Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki