KITABU CHA PILI CHA MAMBO YA NYAKATI
1 Sulemani mwana wa Daudi alizidi kuimarika katika utawala wake, na Yehova Mungu wake alikuwa pamoja naye, akamfanya kuwa mkuu sana.+
2 Sulemani aliagiza Waisraeli wote wakusanywe, wakuu wa maelfu na wa mamia, waamuzi, na viongozi wote wa Israeli, viongozi wa koo.* 3 Kisha Sulemani na Waisraeli wote wakaenda mahali pa juu kule Gibeoni,+ kwa maana hema la mkutano la Mungu wa kweli lilikuwa huko, hema ambalo Musa mtumishi wa Yehova alitengeneza nyikani. 4 Hata hivyo, Daudi alikuwa amelipandisha Sanduku la Mungu wa kweli kutoka Kiriath-yearimu+ na kulileta mahali ambapo Daudi alikuwa ametayarisha kwa ajili yake; alikuwa amepiga hema kwa ajili ya Sanduku hilo huko Yerusalemu.+ 5 Na ile madhabahu ya shaba+ ambayo Bezaleli+ mwana wa Uri mwana wa Huru alikuwa ametengeneza ilikuwa imewekwa mbele ya hema la ibada la Yehova; na Sulemani na Waisraeli wote walikuwa wakisali mbele yake.* 6 Kisha Sulemani akamtolea Yehova dhabihu mahali hapo, alitoa dhabihu 1,000 za kuteketezwa kwenye madhabahu ya shaba+ ya hema la mkutano.
7 Usiku huo Mungu akamtokea Sulemani na kumwambia: “Niombe unachotaka nikupe.”+ 8 Basi Sulemani akamwambia Mungu: “Umemtendea Daudi+ baba yangu kwa upendo mwingi mshikamanifu, nawe umeniweka kuwa mfalme baada yake.+ 9 Sasa, Ee Yehova Mungu, ahadi uliyompa Daudi baba yangu na ithibitike kuwa ya uaminifu,+ kwa maana umeniweka kuwa mfalme juu ya watu wengi sana kama chembe za mavumbi ya dunia.+ 10 Sasa nipe hekima na ujuzi+ ili niwaongoze watu hawa,* kwa maana ni nani anayeweza kulihukumu taifa hili lako lililo kubwa?”+
11 Kisha Mungu akamwambia Sulemani: “Kwa sababu moyo wako unatamani jambo hilo, nawe hukuomba mali, utajiri, wala heshima wala hukuomba wale wanaokuchukia wafe, wala hukuomba maisha marefu,* lakini umeomba hekima na ujuzi ili uwahukumu watu wangu ambao nimekuweka uwe mfalme wao,+ 12 nitakupa hekima na ujuzi; lakini nitakupa pia mali na utajiri na heshima, kuliko mfalme yeyote kabla yako na mfalme yeyote baada yako.”+
13 Basi Sulemani akatoka mahali pa juu huko Gibeoni,+ kutoka mbele ya hema la mkutano, akaja Yerusalemu; naye akatawala Israeli. 14 Sulemani akaendelea kukusanya magari ya vita na farasi;* akawa na magari 1,400 ya vita na farasi* 12,000,+ naye aliwaweka katika majiji ya magari ya vita+ karibu naye huko Yerusalemu.+ 15 Mfalme alifanya fedha na dhahabu huko Yerusalemu iwe nyingi kama mawe,+ na mbao za mierezi ziwe nyingi kama mikuyu katika Shefela.+ 16 Farasi wa Sulemani waliletwa kutoka Misri,+ na wafanyabiashara wa mfalme walinunua makundi ya farasi* kwa bei moja.+ 17 Kila gari kutoka Misri lilinunuliwa kwa vipande 600 vya fedha, na farasi alinunuliwa kwa vipande 150; kisha waliwauzia wafalme wote wa Wahiti na wafalme wa Siria.
2 Basi Sulemani akaagiza nyumba ijengwe kwa ajili ya jina la Yehova+ na nyumba* kwa ajili ya ufalme wake.+ 2 Sulemani akawaandikisha wanaume 70,000 kuwa vibarua,* wanaume 80,000 kuwa wakataji wa mawe milimani,+ na wanaume 3,600 kuwa waangalizi wao.+ 3 Pia, Sulemani akamtumia Hiramu+ mfalme wa Tiro ujumbe huu: “Nifanyie kama ulivyomfanyia Daudi baba yangu ulipomletea mbao za mierezi ili ajenge nyumba ya* kuishi.+ 4 Sasa ninajenga nyumba kwa ajili ya jina la Yehova Mungu wangu, ili niitakase kwake, nifukize uvumba wenye manukato+ mbele zake, na pia kwa ajili ya mikate ya tabaka* inayotolewa daima+ na pia dhabihu za kuteketezwa, asubuhi na jioni,+ nyakati za Sabato,+ miezi mipya,+ na kwenye majira ya sherehe+ za Yehova Mungu wetu. Huu ni wajibu wa kudumu kwa Waisraeli. 5 Nyumba nitakayojenga itakuwa kuu, kwa maana Mungu wetu ni mkuu kuliko miungu mingine yote. 6 Na ni nani anayeweza kumjengea nyumba? Kwa maana mbingu na mbingu za mbingu haziwezi kumtosha,+ basi mimi ni nani hivi kwamba nimjengee nyumba isipokuwa iwe mahali pa kufukizia moshi wa dhabihu mbele zake? 7 Sasa niletee fundi aliye na ustadi wa kutengeneza vitu kwa kutumia dhahabu, fedha, shaba,+ chuma, sufu ya zambarau, nyuzi nyekundu, na nyuzi za bluu, na ambaye anajua kuchonga. Atafanya kazi Yuda na Yerusalemu pamoja na mafundi wangu stadi, ambao Daudi baba yangu aliwachagua.+ 8 Nawe uniletee mbao za mierezi, miberoshi,+ na misandali+ kutoka Lebanoni, kwa maana najua vizuri kwamba watumishi wako wana uzoefu wa kukata miti ya Lebanoni.+ Watumishi wangu watafanya kazi pamoja na watumishi wako+ 9 ili wanitayarishie mbao nyingi sana, kwa maana nyumba nitakayojenga itakuwa na ukuu usio wa kawaida. 10 Sasa tazama! Nitawaletea chakula watumishi wako,+ yaani, wapasua mbao wanaokata miti: nitawaletea kori 20,000 za ngano, kori 20,000* za shayiri, bathi 20,000 za divai, na bathi 20,000* za mafuta.”
11 Ndipo Hiramu mfalme wa Tiro akatuma barua hii kwa Sulemani: “Kwa sababu Yehova anawapenda watu wake, amekuweka kuwa mfalme wao.” 12 Kisha Hiramu akasema: “Na asifiwe Yehova Mungu wa Israeli, aliyeziumba mbingu na dunia, kwa sababu amempa Mfalme Daudi mwana mwenye hekima,+ aliyebarikiwa kuwa na busara na uelewaji,+ atakayejenga nyumba kwa ajili ya Yehova na nyumba kwa ajili ya ufalme wake. 13 Sasa namtuma fundi stadi, aliyebarikiwa kuwa na uelewaji, Hiram-abi,+ 14 mwana wa mwanamke wa kabila la Dani, lakini baba yake alikuwa Mtiro; ana uzoefu wa kutengeneza vitu kwa kutumia dhahabu, fedha, shaba, chuma, mawe, mbao, sufu ya zambarau, nyuzi za bluu, kitambaa bora, na nyuzi nyekundu.+ Anaweza kuchonga michongo ya kila aina na kubuni na kutengeneza kitu chochote anachoambiwa.+ Atafanya kazi pamoja na mafundi wako stadi na mafundi stadi wa bwana wangu Daudi baba yako. 15 Sasa bwana wangu tutumie ngano, shayiri, mafuta, na divai uliyotuahidi sisi watumishi wako.+ 16 Nasi tutakata miti kutoka Lebanoni,+ idadi yoyote unayohitaji, nasi tutakuletea magogo hayo yakiwa mafungu-mafungu ili yaelee baharini mpaka Yopa;+ nawe utayapeleka Yerusalemu.”+
17 Kisha Sulemani akawahesabu wanaume wote waliokuwa wakaaji wageni katika nchi ya Israeli,+ baada ya ile hesabu ya watu ambayo Daudi baba yake alikuwa amechukua,+ wakapatikana wanaume 153,600. 18 Kwa hiyo akawaweka watu 70,000 kati yao kuwa vibarua,* 80,000 kuwa wakataji wa mawe+ milimani, na 3,600 kuwa waangalizi wa kuhakikisha kwamba watu wanafanya kazi.+
3 Kisha Sulemani akaanza kujenga nyumba ya Yehova+ huko Yerusalemu juu ya Mlima Moria,+ mahali ambapo Yehova alikuwa amemtokea Daudi baba yake,+ mahali ambapo Daudi alikuwa ametayarisha kwenye uwanja wa kupuria wa Ornani Myebusi.+ 2 Alianza kujenga siku ya pili ya mwezi wa pili, katika mwaka wa nne wa utawala wake. 3 Na msingi ambao Sulemani aliweka kwa ajili ya ujenzi wa nyumba ya Mungu wa kweli ulikuwa na urefu wa mikono 60 na upana wa mikono 20,+ kulingana na kipimo cha awali.* 4 Ukumbi wa mbele ulikuwa na urefu wa mikono 20, nao ulilingana na upana wa nyumba,* na kimo chake kilikuwa 120;* naye akafunika upande wa ndani kwa dhahabu safi.+ 5 Alifunika nyumba kuu kwa mbao za miberoshi, kisha akaifunika kwa dhahabu bora,+ halafu akaipamba kwa michongo ya mitende+ na minyororo.+ 6 Pia, aliifunika nyumba hiyo kwa mawe maridadi yenye thamani;+ na dhahabu+ aliyotumia ilikuwa dhahabu kutoka Parvaimu. 7 Aliifunika nyumba, maboriti, vizingiti, kuta zake, na milango yake kwa dhahabu;+ naye akachonga makerubi kwenye kuta zake.+
8 Kisha akajenga chumba cha Patakatifu Zaidi;*+ urefu wake ulilingana na upana wa nyumba, mikono 20, na upana wake ulikuwa mikono 20. Akaifunika kwa talanta 600* za dhahabu bora.+ 9 Uzito wa dhahabu iliyotumiwa kutengenezea misumari ulikuwa shekeli 50;* naye alifunika vyumba vya darini kwa dhahabu.
10 Kisha akatengeneza mifano ya makerubi wawili katika chumba cha Patakatifu Zaidi,* akawafunika kwa dhahabu.+ 11 Kwa ujumla mabawa ya makerubi hao+ yalikuwa na urefu wa mikono 20; bawa moja la kerubi wa kwanza lilikuwa na urefu wa mikono mitano nalo liligusa ukuta wa nyumba, na bawa la pili lilikuwa na urefu wa mikono mitano nalo liligusa bawa moja la kerubi wa pili. 12 Na bawa moja la kerubi wa pili lilikuwa na urefu wa mikono mitano nalo liligusa ukuta wa nyumba, na bawa la pili lilikuwa na urefu wa mikono mitano nalo liligusa bawa moja la yule kerubi wa kwanza. 13 Mabawa ya makerubi hao yalikuwa yamenyooshwa kufikia urefu wa mikono 20; nao walikuwa wamesimama kwa miguu yao, nyuso zao zikielekea ndani.*
14 Alitengeneza pia pazia+ kwa nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa chekundu, na kitambaa bora, na kulitarizi kwa mifano ya makerubi.+
15 Kisha akatengeneza nguzo mbili+ mbele ya nyumba hiyo, zenye urefu wa mikono 35, na kifuniko kilichokuwa juu ya kila nguzo kilikuwa na urefu wa mikono mitano.+ 16 Pia alitengeneza minyororo iliyokuwa kama mikufu, akaiweka juu ya nguzo hizo, kisha akatengeneza makomamanga 100 na kuyaweka kwenye minyororo hiyo. 17 Akasimamisha nguzo hizo mbele ya hekalu, moja upande wa kulia* na nyingine upande wa kushoto;* akaiita nguzo ya upande wa kulia Yakini* na nguzo ya upande wa kushoto Boazi.*
4 Kisha akatengeneza madhabahu ya shaba+ yenye urefu wa mikono 20, upana wa mikono 20, na kimo cha mikono 10.
2 Alitengeneza Bahari*+ kwa madini yaliyoyeyushwa. Ilikuwa ya mviringo, yenye upana wa mikono 10 ukingo hadi ukingo na kimo cha mikono 5, na ingeweza kuzungukwa na kamba yenye urefu wa mikono 30.+ 3 Na chini yake kulikuwa na mapambo ya vibuyu,+ ambayo yalizunguka ukingo wote, vibuyu kumi kwa kila mkono mmoja kuzunguka Bahari yote. Vibuyu hivyo vilikuwa katika safu mbili, navyo vilitengenezwa kwa kuyeyushwa vikiwa sehemu ya Bahari hiyo. 4 Ilikuwa juu ya ng’ombe dume 12,+ watatu walitazama kaskazini, watatu walitazama magharibi, watatu walitazama kusini, na watatu walitazama mashariki; na Bahari hiyo ilikuwa juu yao, na sehemu zao zote za nyuma zilielekea katikati. 5 Na unene wake ulikuwa upana wa kiganja kimoja;* na ukingo wake ulitengenezwa kama ukingo wa kikombe, kama ua la yungiyungi. Ingeweza kujaa maji kiasi cha bathi 3,000.*
6 Pia, alitengeneza mabeseni kumi ya kuoshea, akaweka matano upande wa kulia na matano upande wa kushoto.+ Waliyatumia kuoshea vitu vilivyotumiwa kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa.+ Lakini Bahari ilitumiwa na makuhani kuogea.+
7 Kisha alitengeneza vinara kumi vya taa vya dhahabu,+ kulingana na maagizo,+ akaviweka hekaluni, vitano upande wa kulia na vitano upande wa kushoto.+
8 Alitengeneza pia meza kumi na kuziweka hekaluni, tano upande wa kulia na tano upande wa kushoto;+ naye alitengeneza mabakuli 100 ya dhahabu.
9 Kisha akatengeneza ua+ wa makuhani+ na ule ua mkuu+ na milango ya ua huo, akaifunika milango hiyo kwa shaba. 10 Akaiweka ile Bahari upande wa kulia, kuelekea kusini mashariki.+
11 Hiramu alitengeneza pia ndoo za kuondolea majivu, pia sepetu, na mabakuli.+
Basi Hiramu akamaliza kazi yote aliyomfanyia Mfalme Sulemani kuhusiana na nyumba ya Mungu wa kweli:+ 12 zile nguzo mbili+ na vifuniko vyenye umbo la bakuli vilivyokuwa juu ya nguzo hizo; na nyavu mbili+ za kufunika vifuniko hivyo viwili vyenye umbo la bakuli vilivyokuwa juu ya nguzo hizo; 13 yale makomamanga 400+ kwa ajili ya zile nyavu mbili, safu mbili za makomamanga kwa ajili ya kila wavu, ili kufunika vile vifuniko viwili vyenye umbo la bakuli vilivyokuwa juu ya zile nguzo;+ 14 yale magari* kumi na yale mabeseni kumi yaliyokuwa juu ya magari hayo;+ 15 ile Bahari na wale ng’ombe dume 12 waliokuwa chini yake;+ 16 na ndoo za kuondolea majivu, sepetu, nyuma,*+ na vyombo vingine vyote ambavyo Hiram-abivu+ alimtengenezea Mfalme Sulemani kwa shaba iliyong’arishwa kwa ajili ya nyumba ya Yehova. 17 Mfalme alivitengeneza katika kalibu za udongo wa mfinyanzi katika wilaya ya Yordani kwenye eneo lenye udongo mwingi wa mfinyanzi, kati ya Sukothi+ na Sarethani. 18 Sulemani alitengeneza vyombo hivyo vyote kwa wingi sana; uzito wa shaba haukujulikana.+
19 Sulemani alivitengeneza vitu vyote+ vya nyumba ya Mungu wa kweli: madhabahu ya dhahabu;+ meza+ na mikate ya wonyesho iliyokuwa juu ya meza hizo;+ 20 vinara vya taa na taa zake za dhahabu safi,+ ili ziwake mbele ya chumba cha ndani zaidi kulingana na maagizo; 21 na maua, taa, na koleo, vyote vya dhahabu, dhahabu safi kabisa; 22 mikasi ya kukatia tambi za taa, mabakuli, vikombe, na vyetezo, vyote vya dhahabu safi; na lango la nyumba, na milango ya ndani ya Patakatifu Zaidi,+ na milango ya nyumba ya hekalu, ya dhahabu.+
5 Kwa hiyo Sulemani akakamilisha kazi yote aliyopaswa kufanya kwa ajili ya nyumba ya Yehova.+ Kisha Sulemani akaingiza ndani vitu ambavyo Daudi baba yake alikuwa amevifanya kuwa vitakatifu,+ naye akaweka fedha, dhahabu, na vitu vyote katika hazina za nyumba ya Mungu wa kweli.+ 2 Wakati huo Sulemani aliwakusanya wazee wa Israeli, viongozi wote wa makabila, wakuu wa koo* za Israeli. Wakaja Yerusalemu ili kuliondoa sanduku la agano la Yehova katika Jiji la Daudi,+ yaani, Sayuni.+ 3 Wanaume wote wa Israeli walikusanyika mbele ya mfalme wakati wa sherehe* inayofanywa katika mwezi wa saba.+
4 Basi wazee wote wa Israeli wakaja, na Walawi wakalibeba Sanduku.+ 5 Wakalipandisha Sanduku, hema la mkutano,+ na vyombo vyote vitakatifu vilivyokuwa katika hema hilo. Makuhani na Walawi* wakavipandisha vitu hivyo. 6 Mfalme Sulemani na Waisraeli wote waliokusanywa ili wakutane naye walikuwa mbele ya Sanduku. Kondoo na ng’ombe wengi sana wasiohesabika au kujulikana idadi walikuwa wakitolewa dhabihu.+ 7 Kisha makuhani wakalileta sanduku la agano la Yehova mahali pake, katika chumba cha ndani zaidi cha nyumba, yaani, Patakatifu Zaidi, chini ya mabawa ya makerubi.+ 8 Kwa hiyo mabawa ya makerubi yalikuwa yamenyooshwa juu ya mahali ambapo Sanduku liliwekwa, hivi kwamba makerubi hao walilifunika Sanduku na fito zake.+ 9 Fito hizo zilikuwa ndefu sana hivi kwamba ncha zake zilionekana kutoka Patakatifu mbele ya chumba cha ndani zaidi, lakini hazikuonekana kutoka upande wa nje. Nazo ziko huko mpaka leo hii. 10 Hakukuwa na kitu kingine ndani ya Sanduku hilo isipokuwa yale mabamba mawili ambayo Musa aliyaweka humo kule Horebu,+ Yehova alipofanya agano+ na Waisraeli walipokuwa wakitoka Misri.+
11 Makuhani walipotoka mahali patakatifu (kwa maana makuhani wote waliokuwepo walikuwa wamejitakasa,+ bila kuzingatia vikundi vyao),+ 12 waimbaji wote Walawi+ walioongozwa na Asafu,+ Hemani,+ Yeduthuni,+ wana wao na ndugu zao walikuwa wamevaa mavazi ya kitambaa bora, wakiwa wamebeba matoazi, vinanda, na vinubi; walikuwa wamesimama upande wa mashariki wa madhabahu, na makuhani 120 waliokuwa wakipiga tarumbeta walikuwa pamoja nao.+ 13 Mara tu wapiga tarumbeta na waimbaji walipoanza kumsifu na kumshukuru Yehova kwa pamoja, na milio ya tarumbeta, matoazi, na ala nyingine za muziki zilipoanza kusikika walipokuwa wakimsifu Yehova, “kwa maana yeye ni mwema; upendo wake mshikamanifu unadumu milele,”+ ndipo nyumba hiyo, nyumba ya Yehova, ikajaa wingu.+ 14 Makuhani hawakuweza kusimama ili kuhudumu kwa sababu ya wingu hilo, kwa maana utukufu wa Yehova ulijaa katika nyumba ya Mungu wa kweli.+
6 Wakati huo Sulemani alisema: “Yehova alisema kwamba atakaa katika giza zito.+ 2 Sasa nimekujengea nyumba iliyokwezwa, mahali palipofanywa imara ili ukae humo milele.”+
3 Kisha mfalme akageuka na kuanza kulibariki kutaniko lote la Waisraeli huku kutaniko lote la Waisraeli likiwa limesimama.+ 4 Akasema: “Na asifiwe Yehova Mungu wa Israeli, ambaye kwa kinywa chake mwenyewe alimwahidi baba yangu Daudi, na kwa mkono wake mwenyewe ametimiza, akisema, 5 ‘Kuanzia siku niliyowatoa watu wangu nchini Misri, sijachagua jiji katika makabila yote ya Israeli na kujenga humo nyumba ili jina langu likae humo,+ nami sijamchagua mwanamume atakayekuwa kiongozi wa watu wangu Waisraeli. 6 Lakini nimechagua Yerusalemu+ ili jina langu likae humo, nami nimemchagua Daudi awatawale watu wangu Waisraeli.’+ 7 Na moyo wa Daudi baba yangu ulitamani kujenga nyumba kwa ajili ya jina la Yehova Mungu wa Israeli.+ 8 Lakini Yehova akamwambia Daudi baba yangu, ‘Moyo wako ulitamani kujenga nyumba kwa ajili ya jina langu, na ulifanya vizuri kutamani jambo hilo moyoni mwako. 9 Hata hivyo, hutajenga nyumba hiyo, lakini mwana wako mwenyewe utakayemzaa* ndiye atakayeijenga nyumba hiyo kwa ajili ya jina langu.’+ 10 Yehova ametimiza ahadi hiyo aliyoitoa, kwa maana nimechukua mahali pa baba yangu Daudi na kuketi kwenye kiti cha ufalme cha Israeli,+ kama Yehova alivyoahidi.+ Pia nimejenga nyumba kwa ajili ya jina la Yehova Mungu wa Israeli, 11 na humo nimeliweka Sanduku lenye agano+ ambalo Yehova alifanya na Waisraeli.”
12 Kisha akasimama mbele ya madhabahu ya Yehova mbele ya kutaniko lote la Waisraeli, akanyoosha mikono yake.+ 13 (Kwa maana Sulemani alikuwa amejenga jukwaa la shaba na kuliweka katikati ya ua.+ Lilikuwa na urefu wa mikono mitano,* upana wa mikono mitano, na kimo cha mikono mitatu; akasimama juu yake.) Akapiga magoti mbele ya kutaniko lote la Waisraeli na kunyoosha mikono yake kuelekea mbinguni,+ 14 akasema: “Ee Yehova Mungu wa Israeli, hakuna Mungu kama wewe mbinguni wala duniani, unayeshika agano na kuwatendea kwa upendo mshikamanifu watumishi wako wanaotembea mbele zako kwa moyo wao wote.+ 15 Umetimiza ahadi uliyomwahidi mtumishi wako Daudi baba yangu.+ Ulitoa ahadi hiyo kwa kinywa chako mwenyewe, na siku ya leo umeitimiza kwa mkono wako mwenyewe.+ 16 Na sasa, Ee Yehova Mungu wa Israeli, timiza ahadi uliyomwahidi mtumishi wako Daudi baba yangu ulipomwambia, ‘Hutakosa kamwe mwanamume wa uzao wako atakayeketi kwenye kiti cha ufalme cha Israeli mbele zangu, ikiwa tu wana wako watakazia uangalifu njia yao kwa kutembea katika sheria yangu,+ kama ulivyotembea mbele zangu.’+ 17 Na sasa, Ee Yehova Mungu wa Israeli, acha ahadi uliyomwahidi mtumishi wako Daudi baba yangu ithibitike kuwa ya kweli.
18 “Lakini Ee Mungu, je, kweli utakaa duniani pamoja na wanadamu?+ Tazama! Mbingu, naam, mbingu za mbingu, haziwezi kukutosha;+ sembuse nyumba hii niliyoijenga!+ 19 Sasa sikiliza sala yangu mimi mtumishi wako na ombi langu la kutaka kibali, Ee Yehova Mungu wangu, sikiliza kilio changu cha kuomba msaada na sala ambayo mimi mtumishi wako ninasali mbele zako. 20 Macho yako na yatazame nyumba hii usiku na mchana, yatazame mahali ambapo ulisema kwamba utaweka jina lako,+ ili usikilize sala ambayo mimi mtumishi wako ninasali kuelekea mahali hapa. 21 Nawe usikilize sihi zangu mimi mtumishi wako za kuomba msaada na sihi za watu wako Waisraeli wanaposali kuelekea mahali hapa,+ nawe usikilize katika makao yako, kutoka mbinguni;+ naam, usikilize na kusamehe.+
22 “Mwanadamu akimtendea dhambi mwanadamu mwenzake, naye aapishwe* na kuwekwa chini ya wajibu wa kiapo hicho,* naye akiwa chini ya kiapo* aje mbele ya madhabahu yako katika nyumba hii,+ 23 basi usikie kutoka mbinguni na kuchukua hatua na kuwahukumu watumishi wako kwa kumlipa mwovu na kumwadhibu kwa sababu ya jambo alilotenda*+ na kumtangaza mwadilifu kuwa asiye na hatia* na kumthawabisha kulingana na uadilifu wake mwenyewe.+
24 “Na watu wako Waisraeli wakishindwa na maadui kwa sababu ya kuzidi kukutendea dhambi,+ nao warudi na kulitukuza jina lako+ na kusali+ na kukusihi wapate kibali mbele zako katika nyumba hii,+ 25 basi usikie kutoka mbinguni+ na kuwasamehe watu wako Waisraeli dhambi yao na kuwarudisha katika nchi uliyowapa wao na mababu zao.+
26 “Mbingu zikifungwa kusiwe na mvua+ kwa sababu wamezidi kukutendea dhambi,+ nao wasali kuelekea mahali hapa na kulitukuza jina lako na kuacha dhambi yao kwa sababu umewanyenyekeza,*+ 27 basi usikie kutoka mbinguni na kuwasamehe watumishi wako dhambi yao, dhambi ya watu wako Waisraeli, kwa sababu utawafundisha njia nzuri wanayopaswa kutembea ndani yake;+ na ulete mvua+ katika nchi yako ambayo uliwapa watu wako kuwa urithi.
28 “Njaa kali ikitokea nchini,+ au ugonjwa hatari,+ upepo unaochoma, kuvu,+ makundi ya nzige, au parare* wanaokula sana+ au maadui wao wakiwazingira katika jiji lolote nchini*+ au pigo au ugonjwa wa aina yoyote ukitokea,+ 29 sala yoyote,+ ombi lolote la kutaka kibali+ ambalo huenda likatolewa na mtu yeyote au na watu wako wote Waisraeli (kwa sababu kila mmoja anajua mateso yake mwenyewe na maumivu yake mwenyewe)+ wakinyoosha mikono yao kuelekea nyumba hii,+ 30 basi usikie kutoka mbinguni, makao yako,+ nawe usamehe;+ na umthawabishe kila mmoja kulingana na njia zake zote, kwa sababu unajua moyo wake (ni wewe peke yako unayejua vizuri moyo wa mwanadamu),+ 31 ili wakuogope kwa kutembea katika njia zako sikuzote watakazoishi katika nchi uliyowapa mababu zetu.
32 “Pia mgeni ambaye si sehemu ya watu wako Waisraeli na ambaye anatoka katika nchi ya mbali kwa sababu ya jina lako kuu*+ na mkono wako wenye nguvu na mkono wako ulionyooshwa, akija na kusali kuelekea nyumba hii,+ 33 basi usikilize kutoka mbinguni, makao yako, nawe ufanye mambo yote ambayo mgeni huyo anakuomba ufanye, ili watu wote duniani wajue jina lako+ na kukuogopa, kama watu wako Waisraeli wanavyokuogopa, na ili wajue kwamba nyumba hii niliyojenga imeitwa kwa jina lako.
34 “Watu wako wakienda vitani kupigana na maadui wao mahali utakapowaelekeza+ nao wasali+ kwako kuelekea jiji hili ambalo umechagua na kuelekea nyumba ambayo nimejenga kwa ajili ya jina lako,+ 35 basi usikie kutoka mbinguni sala yao na ombi lao la kutaka kibali, nawe utekeleze hukumu kwa ajili yao.+
36 “Wakikutendea dhambi (kwa sababu hakuna mwanadamu asiyetenda dhambi),+ nawe uwakasirikie vikali na kuwaacha mikononi mwa maadui, na waliowateka wawapeleke katika nchi fulani, mbali au karibu,+ 37 nao warudiwe na ufahamu wakiwa katika nchi ya watu waliowachukua mateka, na kukurudia na kukuomba kibali katika nchi walikopelekwa mateka, wakisema, ‘Tumetenda dhambi na kukosea; tumetenda uovu,’+ 38 nao wakurudie kwa moyo wao wote+ na kwa nafsi* yao yote katika nchi walikopelekwa mateka,+ nao wasali kwako kuelekea nchi yao ambayo uliwapa mababu zao na kuelekea jiji ambalo umelichagua+ na nyumba ambayo nimejenga kwa ajili ya jina lako, 39 basi usikie kutoka mbinguni, makao yako, sala yao na ombi lao la kutaka kibali, nawe utekeleze hukumu kwa ajili yao+ na uwasamehe watu wako ambao wamekutendea dhambi.
40 “Sasa, Ee Mungu wangu, tafadhali, macho yako yatazame na masikio yako yasikilize kwa makini sala inayotolewa* mahali hapa.+ 41 Na sasa, Ee Yehova Mungu, panda uingie mahali pako pa kupumzikia,+ wewe pamoja na Sanduku la nguvu zako. Makuhani wako, Ee Yehova Mungu, na wavishwe wokovu, na acha washikamanifu wako washangilie kwa sababu ya wema wako.+ 42 Ee Yehova Mungu, usimkatae* mtiwa-mafuta wako.+ Ukumbuke upendo wako mshikamanifu kwa Daudi mtumishi wako.”+
7 Basi, mara tu Sulemani alipomaliza kusali,+ moto ulishuka kutoka mbinguni+ ukateketeza ile dhabihu ya kuteketezwa na dhabihu nyinginezo, na utukufu wa Yehova ukajaa katika nyumba hiyo.+ 2 Makuhani hawakuweza kuingia ndani ya nyumba ya Yehova kwa sababu utukufu wa Yehova ulikuwa umejaa katika nyumba ya Yehova.+ 3 Waisraeli wote walikuwa wakitazama moto uliposhuka na utukufu wa Yehova ulipokuwa juu ya nyumba hiyo, nao wakainama kifudifudi kwenye sakafu ya mawe, wakasujudu na kumshukuru Yehova, “kwa maana yeye ni mwema; upendo wake mshikamanifu unadumu milele.”
4 Sasa mfalme na watu wote wakazitoa dhabihu mbele za Yehova.+ 5 Mfalme Sulemani alitoa ng’ombe 22,000 na kondoo 120,000 kuwa dhabihu. Basi mfalme na watu wote wakaizindua nyumba ya Mungu wa kweli.+ 6 Makuhani walikuwa wamesimama katika vituo vyao vya kazi, na Walawi pia waliokuwa na ala za muziki zilizopigwa kuambatana na nyimbo ambazo Yehova aliimbiwa.+ (Mfalme Daudi alikuwa ametengeneza ala hizo ili kumshukuru Yehova—“kwa maana upendo wake mshikamanifu unadumu milele”—wakati Daudi alipokuwa akitoa sifa pamoja nao.*) Na makuhani walikuwa wakipiga tarumbeta kwa sauti kubwa+ mbele yao, huku Waisraeli wote wakiwa wamesimama.
7 Kisha Sulemani akatakasa sehemu ya katikati ya ua uliokuwa mbele ya nyumba ya Yehova, kwa maana alipaswa kutolea mahali hapo dhabihu za kuteketezwa+ na vipande vya mafuta vya dhabihu za ushirika, kwa sababu madhabahu ya shaba+ ambayo Sulemani alikuwa amejenga haingeweza kutoshea dhabihu za kuteketezwa, matoleo ya nafaka,+ na vipande vya mafuta.+ 8 Wakati huo Sulemani alifanya sherehe hiyo kwa siku saba+ pamoja na Waisraeli wote, kutaniko kubwa sana kuanzia Lebo-hamathi* kushuka mpaka kwenye Korongo* la Misri.+ 9 Lakini siku ya nane* walifanya kusanyiko takatifu,+ kwa sababu walikuwa wameizindua madhabahu kwa siku saba na kufanya sherehe hiyo kwa siku saba. 10 Kisha siku ya 23 ya mwezi wa saba, aliwaruhusu watu waende nyumbani kwao wakishangilia+ na kufurahi moyoni kwa sababu ya wema ambao Yehova alikuwa amemtendea Daudi na Sulemani na watu wake Waisraeli.+
11 Kwa hiyo Sulemani akaikamilisha nyumba ya Yehova na nyumba ya* mfalme;+ na kila kitu ambacho Sulemani alitamani moyoni mwake kufanya kuhusiana na nyumba ya Yehova na nyumba yake mwenyewe, alifanikiwa kukitimiza.+ 12 Kisha Yehova akamtokea Sulemani+ usiku na kumwambia: “Nimesikia sala yako, nami nimechagua mahali hapa kwa ajili yangu ili pawe nyumba ya dhabihu.+ 13 Nikifunga mbingu ili mvua isinyeshe, nami nikiamuru panzi waile nchi, nami nikileta ugonjwa hatari miongoni mwa watu wangu, 14 na watu wangu ambao wameitwa kwa jina langu+ wakijinyenyekeza+ na kusali na kuutafuta uso wangu na kuacha njia zao ovu,+ ndipo nitakaposikia kutoka mbinguni na kuwasamehe dhambi yao na kuiponya nchi yao.+ 15 Sasa macho yangu yatatazama na masikio yangu yatasikiliza kwa makini sala zinazotolewa mahali hapa.+ 16 Na sasa nimeichagua nyumba hii na kuitakasa ili jina langu likae humu milele,+ na macho yangu na moyo wangu utakuwa humu sikuzote.+
17 “Nawe, ukitembea mbele zangu kama Daudi baba yako alivyotembea, kwa kutenda mambo yote niliyokuamuru, nawe ukitii masharti yangu na sheria* zangu,+ 18 ndipo nitakapoimarisha kiti cha ufalme wako,+ kama nilivyofanya agano pamoja na Daudi baba yako,+ niliposema, ‘Hutakosa kamwe mwanamume wa uzao wako atakayetawala Israeli.’+ 19 Lakini ikiwa utageuka na kuacha maagizo yangu na amri zangu ambazo nimeweka mbele yako, nawe uende na kuabudu miungu mingine na kuiinamia,+ 20 nitawang’oa Waisraeli kutoka katika nchi ambayo nimewapa,+ na nyumba hii ambayo nimeitakasa kwa ajili ya jina langu nitaitupilia mbali kutoka mbele za macho yangu, nami nitaifanya iwe kitu cha kudharauliwa* na kitu cha kudhihakiwa miongoni mwa mataifa yote.+ 21 Na nyumba hii itakuwa marundo ya magofu. Kila mtu atakayepita karibu nayo ataitazama kwa mshangao+ na kuuliza, ‘Kwa nini Yehova aliitendea hivi nchi hii na nyumba hii?’+ 22 Kisha watasema, ‘Ni kwa sababu walimwacha Yehova+ Mungu wa mababu zao, aliyewatoa nchini Misri,+ nao wakashikamana na miungu mingine, wakaiinamia na kuiabudu.+ Ndiyo sababu aliwaletea msiba huo wote.’”+
8 Katika muda wa miaka 20 ambayo Sulemani alijenga nyumba ya Yehova na nyumba yake* mwenyewe,+ 2 Sulemani alijenga upya majiji ambayo Hiramu+ alikuwa amempa, akawapa Waisraeli* waishi humo. 3 Isitoshe, Sulemani alienda Hamath-soba na kuliteka jiji hilo. 4 Kisha akajenga tena jiji la Tadmori kule nyikani na majiji yote yenye maghala+ aliyokuwa amejenga Hamathi.+ 5 Alijenga pia Beth-horoni ya Juu+ na Beth-horoni ya Chini,+ majiji yenye ngome yaliyokuwa na kuta, malango, na makomeo, 6 na Baalathi+ na pia majiji yote ya Sulemani yenye maghala, majiji yote ya magari ya vita,+ majiji ya wapanda farasi, na chochote ambacho Sulemani alitamani kujenga huko Yerusalemu, Lebanoni, na katika nchi yote iliyokuwa chini ya mamlaka yake.
7 Na watu wote waliobaki, yaani, Wahiti, Waamori, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi+ ambao hawakuwa sehemu ya Waisraeli,+ 8 wazao wao waliobaki nchini—wale ambao Waisraeli hawakuwaangamiza+—Sulemani aliwaandikisha ili wafanye kazi ya kulazimishwa mpaka leo hii.+ 9 Lakini Sulemani hakumfanya Mwisraeli yeyote kuwa mtumwa wake,+ kwa sababu walikuwa mashujaa wake, wakuu wa makamanda wake wasaidizi, na wakuu wa waendeshaji wa magari yake ya vita na wapanda farasi wake.+ 10 Kulikuwa na wakuu 250 wa wasaidizi wa Mfalme Sulemani, waliokuwa wasimamizi wa watu.+
11 Pia, Sulemani alimtoa binti ya Farao+ kutoka katika Jiji la Daudi na kumpeleka katika nyumba aliyokuwa amemjengea,+ kwa maana alisema: “Ingawa ni mke wangu, hapaswi kukaa katika nyumba ya Mfalme Daudi wa Israeli, kwa sababu sehemu ambazo Sanduku la Yehova limeletwa ni takatifu.”+
12 Kisha Sulemani akamtolea Yehova dhabihu za kuteketezwa+ kwenye madhabahu+ ya Yehova aliyokuwa amejenga mbele ya ukumbi.+ 13 Alifuata utaratibu wa kila siku kwa kutoa dhabihu kulingana na amri ya Musa iliyohusu Sabato,+ miezi mipya,+ na sherehe zilizoamriwa mara tatu kwa mwaka+—Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu,+ Sherehe ya Majuma,+ na Sherehe ya Vibanda.*+ 14 Pia, alipanga vikundi vya makuhani+ kwa ajili ya utumishi wao kulingana na sheria ya Daudi baba yake, na Walawi katika vituo vyao vya kazi, ili watoe sifa+ na kuhudumu mbele ya makuhani kulingana na utaratibu wa kila siku, na walinzi wa malango katika vikundi vyao kwenye malango mbalimbali,+ kwa maana hivyo ndivyo alivyoamuru Daudi, mtu wa Mungu wa kweli. 15 Nao hawakuacha amri ambayo mfalme aliwapa makuhani na Walawi kuhusiana na jambo lolote au kuhusiana na maghala. 16 Basi kazi yote ya Sulemani ilipangwa vizuri sana,* kuanzia siku ambayo msingi wa nyumba ya Yehova uliwekwa+ mpaka ilipomalizwa. Basi nyumba ya Yehova ikakamilishwa.+
17 Huo ndio wakati ambapo Sulemani alienda Esion-geberi+ na Elothi+ kwenye ufuo wa bahari katika nchi ya Edomu.+ 18 Hiramu+ aliwatuma watumishi wake mwenyewe wampelekee meli na mabaharia wenye uzoefu. Wakaenda Ofiri+ pamoja na watumishi wa Sulemani, wakachukua huko talanta 450* za dhahabu+ na kumletea Mfalme Sulemani.+
9 Basi malkia wa Sheba+ alisikia habari za Sulemani, kwa hiyo akaja Yerusalemu kumjaribu kwa maswali magumu.* Alikuja na msafara wenye kuvutia sana, pamoja na ngamia waliobeba mafuta ya zeri na dhahabu nyingi sana+ na mawe yenye thamani. Akafika mbele ya Sulemani na kumwambia mambo yote yaliyokuwa moyoni mwake.+ 2 Kisha Sulemani akajibu maswali yake yote. Hakuna jambo lolote lililokuwa gumu sana* kwa Sulemani asiweze kumweleza.
3 Malkia wa Sheba alipoona hekima yote ya Sulemani,+ nyumba aliyojenga,+ 4 chakula kilichokuwa mezani pake,+ jinsi watumishi wake walivyoketi, jinsi watumishi wake walivyohudumu mezani na pia mavazi yao, na wale waliompa vinywaji na jinsi walivyovalia, na dhabihu zake za kuteketezwa alizotoa kwa ukawaida katika nyumba ya Yehova,+ alipigwa na bumbuazi.* 5 Basi akamwambia mfalme: “Habari nilizosikia katika nchi yangu kuhusu mafanikio* yako na kuhusu hekima yako zilikuwa za kweli. 6 Lakini sikuamini habari hizo mpaka nilipokuja na kujionea kwa macho yangu mwenyewe.+ Na kwa kweli sikuwa nimeambiwa hata nusu ya hekima yako nyingi.+ Umezidi kwa mbali habari nilizosikia.+ 7 Wenye furaha ni watu wako, na wenye furaha ni watumishi wako wanaosimama mbele yako daima, wakiisikiliza hekima yako! 8 Na asifiwe Yehova Mungu wako, ambaye amependezwa nawe, akakuweka kwenye kiti chake cha ufalme ukiwa mfalme kwa niaba ya Yehova Mungu wako. Kwa sababu Mungu wako anawapenda Waisraeli,+ na ili kuwafanya wadumu milele, alikuweka kuwa mfalme juu yao ili utekeleze haki na uadilifu.”
9 Kisha akampa mfalme talanta 120* za dhahabu+ na kiasi kikubwa sana cha mafuta ya zeri na mawe yenye thamani. Mfalme Sulemani hakuwahi tena kuletewa kiasi kikubwa hivyo cha mafuta ya zeri kama alicholetewa na malkia wa Sheba.+
10 Isitoshe, watumishi wa Hiramu na watumishi wa Sulemani ambao walileta dhahabu kutoka Ofiri,+ walileta pia mbao za misandali na mawe yenye thamani.+ 11 Mfalme alitumia mbao hizo za misandali kutengeneza ngazi za nyumba ya Yehova+ na nyumba ya* mfalme,+ na pia vinubi na vinanda vya waimbaji.+ Mbao kama hizo hazikuwa zimewahi kuonekana katika nchi ya Yuda.
12 Mfalme Sulemani alimpa pia malkia wa Sheba kitu chochote alichotamani na kuomba, zaidi ya* vitu alivyomletea mfalme. Kisha akaondoka na kurudi katika nchi yake, pamoja na watumishi wake.+
13 Na dhahabu iliyoletwa kwa Sulemani katika mwaka mmoja ilikuwa na uzito wa talanta 666 za dhahabu,+ 14 mbali na dhahabu iliyoletwa na wafanyabiashara wasafiri na wauzaji wa bidhaa na wafalme wote wa Uarabuni na magavana wa nchi waliokuwa wakimletea Sulemani dhahabu na fedha.+
15 Mfalme Sulemani alitengeneza ngao kubwa 200 za dhahabu iliyochanganywa na madini mengine+ (kwa kila ngao alitumia shekeli 600* za dhahabu hiyo)+ 16 na ngao ndogo* 300 za dhahabu iliyochanganywa na madini mengine (kwa kila ngao ndogo alitumia mina tatu* za dhahabu). Kisha mfalme akaziweka katika Nyumba ya Msitu wa Lebanoni.+
17 Mfalme pia alitengeneza kiti kikubwa cha ufalme cha pembe za tembo na kukifunika kwa dhahabu safi.+ 18 Kiti hicho cha ufalme kilikuwa na ngazi sita, nacho kiliunganishwa na kiti cha miguu cha dhahabu, na kilikuwa pia na mikono pande zote mbili, na simba wawili+ walisimama kando ya mikono hiyo. 19 Na kulikuwa na simba 12+ waliosimama kwenye ngazi hizo sita, wawili kwenye kila ngazi, mmoja upande huu na mwingine upande wa pili. Hakuna ufalme mwingine wowote uliokuwa umetengeneza kiti kama hicho. 20 Vyombo vyote vya kunywea vya Mfalme Sulemani vilikuwa vya dhahabu, na vyombo vyote vya Nyumba ya Msitu wa Lebanoni vilikuwa vya dhahabu safi. Hakukuwa na kitu chochote kilichotengenezwa kwa fedha, kwa maana fedha ilionwa kuwa si kitu katika siku za Sulemani.+ 21 Kwa maana meli za mfalme zilikuwa zikienda Tarshishi+ na watumishi wa Hiramu.+ Mara moja baada ya kila miaka mitatu, meli za Tarshishi zilikuja zikiwa zimejazwa dhahabu na fedha, pembe za tembo,+ sokwe, na tausi.
22 Kwa hiyo Mfalme Sulemani alikuwa na utajiri mwingi zaidi na hekima kuliko wafalme wengine wote duniani.+ 23 Na wafalme wote duniani walitaka kukutana na* Sulemani ili wasikie hekima yake ambayo Mungu wa kweli alikuwa ameweka moyoni mwake.+ 24 Kila mmoja wao alileta zawadi—vitu vya fedha, vitu vya dhahabu, mavazi,+ silaha, mafuta ya zeri, farasi, na nyumbu—na walifanya hivyo mwaka baada ya mwaka. 25 Na Sulemani alikuwa na mabanda 4,000 kwa ajili ya farasi wake na magari yake ya vita na pia alikuwa na farasi* 12,000,+ naye aliwaweka katika majiji ya magari ya vita karibu naye huko Yerusalemu.+ 26 Naye aliwatawala wafalme wote kuanzia Mto Efrati mpaka nchi ya Wafilisti hadi kwenye mpaka wa Misri.+ 27 Mfalme alifanya fedha huko Yerusalemu iwe nyingi kama mawe, na mbao za mierezi ziwe nyingi kama mikuyu katika Shefela.+ 28 Nao walikuwa wakimletea Sulemani farasi kutoka Misri+ na kutoka katika nchi nyingine zote.
29 Na mambo mengine katika historia ya Sulemani,+ kuanzia mwanzo mpaka mwisho, je, hayajaandikwa katika maandishi ya nabii Nathani,+ katika unabii wa Ahiya+ Mshilo, na katika kumbukumbu ya maono ya mwonaji Ido+ kumhusu Yeroboamu+ mwana wa Nebati? 30 Sulemani alitawala nchi yote ya Israeli kwa miaka 40 akiwa Yerusalemu. 31 Kisha Sulemani akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake. Basi wakamzika katika Jiji la Daudi baba yake;+ na Rehoboamu mwanawe akawa mfalme baada yake.+
10 Rehoboamu alienda Shekemu,+ kwa maana Waisraeli wote walikuwa wamekuja Shekemu kumfanya kuwa mfalme.+ 2 Mara tu Yeroboamu+ mwana wa Nebati aliposikia habari hizo (bado alikuwa akiishi Misri kwa sababu alikuwa amemkimbia Mfalme Sulemani),+ akarudi kutoka Misri. 3 Ndipo wakawatuma watu waende kumwita, kisha Yeroboamu na Waisraeli wote wakaja kwa Rehoboamu na kumwambia hivi: 4 “Baba yako aliifanya nira yetu kuwa nzito.+ Lakini ukiufanya utumishi mzito wa baba yako kuwa mwepesi zaidi na kupunguza nira nzito* aliyotutwika, tutakutumikia.”
5 Ndipo akawaambia: “Rudini kwangu baada ya siku tatu.” Basi watu wakaenda zao.+ 6 Kisha Mfalme Rehoboamu akashauriana na wanaume wazee waliomtumikia Sulemani baba yake alipokuwa hai, akawauliza: “Mnanishauri niwape jibu gani watu hawa?” 7 Wakamjibu: “Ukiwa mwema kwa watu hawa na kuwafurahisha na kuwapa jibu linalofaa, watakuwa watumishi wako sikuzote.”
8 Hata hivyo, alikataa ushauri aliopewa na wanaume wazee, akashauriana na vijana wa rika lake na ambao sasa walikuwa watumishi wake.+ 9 Aliwauliza: “Mnashauri tuwape jibu gani watu hawa ambao wameniambia, ‘Ifanye nira ambayo baba yako alitutwika iwe nyepesi zaidi’?” 10 Vijana hao wa rika lake wakamwambia: “Hivi ndivyo unavyopaswa kuwaambia watu waliokwambia, ‘Baba yako aliifanya nira yetu kuwa nzito, lakini wewe unapaswa kuifanya kuwa nyepesi zaidi kwa ajili yetu’; hivi ndivyo unavyopaswa kuwaambia, ‘Kidole changu kidogo kitakuwa kinene kuliko kiuno cha baba yangu. 11 Baba yangu aliwatwika nira nzito, lakini mimi nitazidisha uzito wa nira yenu. Baba yangu aliwaadhibu kwa mijeledi, lakini mimi nitawaadhibu kwa mijeledi yenye miiba.’”
12 Yeroboamu na watu wote wakaja kwa Rehoboamu siku ya tatu, kama mfalme alivyokuwa amesema: “Rudini kwangu siku ya tatu.”+ 13 Lakini mfalme akawajibu kwa ukali. Kwa hiyo Mfalme Rehoboamu akakataa ushauri wa wanaume wazee. 14 Akawajibu kama alivyoshauriwa na vijana wa rika lake, na kusema: “Nitafanya nira yenu iwe nzito zaidi, nami nitazidisha uzito wake. Baba yangu aliwaadhibu kwa mijeledi, lakini mimi nitawaadhibu kwa mijeledi yenye miiba.” 15 Basi mfalme hakuwasikiliza watu, kwa sababu Mungu wa kweli ndiye aliyesababisha badiliko hilo la mambo,+ ili atimize neno ambalo Yehova alimwambia Yeroboamu mwana wa Nebati kupitia Ahiya Mshilo.+
16 Waisraeli wote walipoona kwamba mfalme amekataa kuwasikiliza, wakamwambia hivi mfalme: “Tuna ushirika gani na Daudi? Hatuna urithi wowote katika mwana wa Yese. Kila mtu aende kwa miungu yake, enyi Waisraeli! Sasa itunze nyumba yako mwenyewe, Ee Daudi.”+ Ndipo Waisraeli wote wakarudi katika nyumba zao.*+
17 Lakini Rehoboamu akaendelea kuwatawala Waisraeli walioishi katika majiji ya Yuda.+
18 Kisha Mfalme Rehoboamu akamtuma Hadoramu,+ aliyekuwa msimamizi wa watu waliofanya kazi ya kulazimishwa, lakini Waisraeli wote wakamuua kwa kumpiga mawe. Mfalme Rehoboamu akafaulu kupanda gari lake na kukimbilia Yerusalemu.+ 19 Na tangu siku hiyo Waisraeli wamekuwa wakiiasi nyumba ya Daudi.
11 Rehoboamu alipofika Yerusalemu, mara moja aliikusanya nyumba ya Yuda na kabila la Benjamini,+ mashujaa 180,000 waliozoezwa,* ili wapigane na Waisraeli na kuurudisha ufalme kwa Rehoboamu.+ 2 Kisha neno hili la Yehova likamjia Shemaya+ mtu wa Mungu wa kweli: 3 “Mwambie Rehoboamu mwana wa Sulemani mfalme wa Yuda na Waisraeli wote walio Yuda na Benjamini, 4 ‘Hivi ndivyo Yehova anavyosema: “Msipande kwenda kupigana na ndugu zenu. Kila mmoja wenu arudi nyumbani kwake, kwa maana nimesababisha mambo haya yatukie.”’”+ Basi wakalitii neno la Yehova na kurudi, nao hawakwenda kupigana na Yeroboamu.
5 Rehoboamu aliishi Yerusalemu na kujenga majiji yenye ngome huko Yuda. 6 Basi akajenga* Bethlehemu,+ Etamu, Tekoa,+ 7 Beth-suri, Soko,+ Adulamu,+ 8 Gathi,+ Maresha, Zifu,+ 9 Adoraimu, Lakishi,+ Azeka,+ 10 Sora, Aiyaloni,+ na Hebroni,+ majiji yenye ngome yaliyokuwa Yuda na Benjamini. 11 Pia, aliimarisha maeneo yenye ngome, akawaweka makamanda humo na kuwapa chakula na mafuta na divai, 12 naye akapeleka ngao kubwa na mikuki katika majiji yote mbalimbali; akayaimarisha kwa kiwango kikubwa sana. Na majiji ya Yuda na Benjamini yakaendelea kuwa yake.
13 Na makuhani na Walawi waliokuwa katika nchi yote ya Israeli wakamuunga mkono, wakaja kutoka katika maeneo yao yote. 14 Walawi waliacha malisho yao na miliki yao+ wakaja Yuda na Yerusalemu, kwa sababu Yeroboamu na wanawe walikuwa wamewaondoa ili wasiwe makuhani wa Yehova.+ 15 Kisha Yeroboamu akawaweka makuhani wake mwenyewe ili wahudumu mahali pa juu+ na kuwatumikia roho waovu wenye umbo la mbuzi*+ na ndama aliokuwa ametengeneza.+ 16 Na watu kutoka katika makabila yote ya Israeli waliokuwa wameazimia moyoni mwao kumtafuta Yehova Mungu wa Israeli wakawafuata mpaka Yerusalemu ili kumtolea dhabihu Yehova Mungu wa mababu zao.+ 17 Kwa miaka mitatu waliuimarisha ufalme wa Yuda na kumuunga mkono Rehoboamu mwana wa Sulemani, kwa maana walitembea katika njia ya Daudi na Sulemani kwa miaka mitatu.
18 Kisha Rehoboamu akamwoa Mahalathi binti ya Yerimothi mwana wa Daudi na wa Abihaili binti ya Eliabu+ mwana wa Yese. 19 Baada ya muda akamzalia wana hawa: Yeushi, Shemaria, na Zahamu. 20 Kisha akamwoa Maaka mjukuu wa Absalomu.+ Baada ya muda akamzalia Abiya,+ Atai, Ziza, na Shelomithi. 21 Rehoboamu alimpenda zaidi Maaka mjukuu wa Absalomu kuliko wake zake wengine wote na masuria+ wake, kwa maana alikuwa na wake 18 na masuria 60, naye akawazaa wana 28 na mabinti 60. 22 Kwa hiyo Rehoboamu akamweka Abiya mwana wa Maaka kuwa mkuu na kiongozi miongoni mwa ndugu zake, kwa maana alikusudia kumweka kuwa mfalme. 23 Hata hivyo, alitenda kwa busara* na kuwatuma* baadhi ya wanawe kwenye maeneo yote ya Yuda na Benjamini, kwenye majiji yote yenye ngome,+ akawapa chakula kingi na kuwatafutia wake wengi.
12 Mara tu baada ya utawala wa Rehoboamu kuimarika kabisa,+ naye akawa na nguvu, aliiacha Sheria ya Yehova,+ na Waisraeli wote pia wakaiacha. 2 Katika mwaka wa tano wa utawala wa Mfalme Rehoboamu, Mfalme Shishaki+ wa Misri alishambulia Yerusalemu, kwa maana hawakuwa waaminifu kwa Yehova. 3 Alikuwa na magari 1,200 ya vita, wapanda farasi 60,000, na idadi isiyohesabika ya wanajeshi waliokuja pamoja naye kutoka Misri—Walibya, Wasukii, na Waethiopia.+ 4 Aliyateka majiji yenye ngome ya Yuda na mwishowe akafika Yerusalemu.
5 Nabii Shemaya+ akaja kwa Rehoboamu na wakuu wa Yuda waliokuwa wamekusanyika Yerusalemu kwa sababu ya Shishaki, akawaambia: “Yehova anasema hivi, ‘Mmeniacha mimi, nami pia nimewaacha ninyi mikononi+ mwa Shishaki.’” 6 Ndipo wakuu wa Israeli na mfalme wakajinyenyekeza+ na kusema: “Yehova ni mwadilifu.” 7 Yehova alipoona kwamba wamejinyenyekeza, neno la Yehova likamjia Shemaya likisema: “Wamejinyenyekeza. Sitawaangamiza,+ na baada ya muda mfupi nitawaokoa. Sitalimwagia jiji la Yerusalemu ghadhabu yangu kupitia Shishaki. 8 Lakini watakuwa watumishi wake, ili wajue tofauti kati ya kunitumikia mimi na kuwatumikia wafalme wa* nchi nyingine.”
9 Basi Mfalme Shishaki wa Misri akashambulia Yerusalemu. Akachukua hazina za nyumba ya Yehova+ na hazina za nyumba ya* mfalme. Alichukua kila kitu, kutia ndani ngao za dhahabu ambazo Sulemani alikuwa ametengeneza.+ 10 Basi Mfalme Rehoboamu akatengeneza ngao za shaba zichukue mahali pa ngao hizo, akaziweka chini ya ulinzi wa mkuu wa walinzi,* aliyelinda mlango wa nyumba ya mfalme. 11 Wakati wowote ambapo mfalme alikuja katika nyumba ya Yehova, walinzi waliingia ndani na kuzichukua, kisha walizirudisha katika chumba cha walinzi. 12 Kwa sababu mfalme alijinyenyekeza, hasira ya Yehova iliacha kuwaka dhidi yake,+ naye hakuwaangamiza kabisa.+ Isitoshe, kulikuwa na mambo fulani mema yaliyopatikana nchini Yuda.+
13 Mfalme Rehoboamu aliimarisha mamlaka yake jijini Yerusalemu na kuendelea kutawala; Rehoboamu alikuwa na umri wa miaka 41 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 17 huko Yerusalemu, jiji ambalo Yehova alichagua miongoni mwa makabila yote ya Israeli ili kuweka jina lake humo. Mama yake aliitwa Naama, naye alikuwa Mwamoni.+ 14 Lakini alitenda maovu, kwa maana hakuwa ameazimia moyoni mwake kumtafuta Yehova.+
15 Na historia ya Rehoboamu, kuanzia mwanzo mpaka mwisho, je, haijaandikwa katika maandishi ya nabii Shemaya+ na mwonaji Ido+ katika kumbukumbu za ukoo? Kulikuwa na vita daima kati ya Rehoboamu na Yeroboamu.+ 16 Kisha Rehoboamu akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi;+ na Abiya+ mwanawe akawa mfalme baada yake.
13 Katika mwaka wa 18 wa utawala wa Mfalme Yeroboamu, Abiya akawa mfalme wa Yuda.+ 2 Alitawala kwa miaka mitatu huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Mikaya+ binti ya Urieli wa Gibea.+ Na kulikuwa na vita kati ya Abiya na Yeroboamu.+
3 Basi Abiya akaenda vitani akiwa na jeshi lenye mashujaa hodari 400,000 waliozoezwa.*+ Na Yeroboamu akajipanga kivita ili kupigana naye akiwa na wanaume 800,000, mashujaa hodari waliozoezwa.* 4 Sasa Abiya akasimama juu ya Mlima Semaraimu, katika eneo lenye milima la Efraimu, akasema: “Nisikilizeni, Ee Yeroboamu na Waisraeli wote. 5 Je, hamjui kwamba Yehova Mungu wa Israeli alimpa Daudi ufalme juu ya Israeli milele,+ yeye na wanawe,+ kupitia agano la chumvi?*+ 6 Lakini Yeroboamu+ mwana wa Nebati, mtumishi wa Sulemani mwana wa Daudi, akainuka na kumwasi bwana wake.+ 7 Na wanaume wazembe, wasiofaa kitu wakaendelea kujiunga naye. Nao walimzidi maarifa Rehoboamu mwana wa Sulemani, Rehoboamu alipokuwa kijana mchanga asiye na ujasiri, naye hangeweza kushindana nao.
8 “Na sasa mnafikiri kwamba mnaweza kushindana na ufalme wa Yehova ulio mikononi mwa wana wa Daudi kwa sababu ninyi ni umati mkubwa nanyi mna ndama wa dhahabu ambao Yeroboamu aliwatengenezea wawe miungu yenu.+ 9 Je, hamjawafukuza makuhani wa Yehova,+ wazao wa Haruni, na Walawi, na je, hamjawaweka makuhani wenu wenyewe kama yalivyofanya mataifa ya nchi nyingine?+ Yeyote aliyeleta* ng’ombe dume mchanga na kondoo dume saba, angeweza kuwa kuhani wa vitu ambavyo si miungu. 10 Lakini sisi, Yehova ndiye Mungu wetu,+ nasi hatujamwacha; makuhani wetu, wazao wa Haruni, wanamhudumia Yehova, na Walawi wanawasaidia kazi. 11 Wanamfukizia Yehova moshi wa dhabihu za kuteketezwa kila asubuhi na kila jioni+ pamoja na uvumba uliotiwa manukato,+ na mikate ya tabaka*+ iko kwenye meza iliyotengenezwa kwa dhahabu safi, nao wanawasha kinara cha taa cha dhahabu+ na taa zake kila jioni,+ kwa sababu tunatekeleza jukumu letu kwa Yehova Mungu wetu; lakini ninyi mmemwacha. 12 Sasa tazama! Mungu wa kweli yuko pamoja nasi, akituongoza, na makuhani wake wakiwa na tarumbeta za kutoa ishara ya vita dhidi yenu. Enyi wanaume wa Israeli, msipigane na Yehova Mungu wa mababu zenu, kwa maana hamtafanikiwa.”+
13 Lakini Yeroboamu alituma wanajeshi wawavizie kutoka nyuma, hivi kwamba jeshi lake lilikabili Yuda upande wa mbele na wanajeshi waliovizia walikuwa nyuma yao. 14 Wanaume wa Yuda walipogeuka, waligundua kwamba wanashambuliwa kutoka mbele na nyuma. Kwa hiyo wakaanza kumlilia Yehova,+ huku makuhani wakipiga tarumbeta kwa sauti kubwa. 15 Wanaume wa Yuda wakaanza kupiga kelele za vita, na wanaume hao wa Yuda walipopiga kelele za vita, Mungu wa kweli akamshinda Yeroboamu na Waisraeli wote mbele ya Abiya na Yuda. 16 Waisraeli wakawakimbia wanaume wa Yuda, na Mungu akawatia mikononi mwao. 17 Abiya na watu wake wakawachinja wanajeshi wengi, wakaendelea kuwaua wanajeshi wa Israeli, waliwaua wanaume 500,000 waliozoezwa.* 18 Basi wanaume wa Israeli wakanyenyekezwa wakati huo, lakini wanaume wa Yuda waliwashinda kwa sababu walimtegemea* Yehova Mungu wa mababu zao.+ 19 Abiya akaendelea kumfuatia Yeroboamu, akateka majiji yake, Betheli+ na miji yake, Yeshana na miji yake, na Efraini+ na miji yake. 20 Na Yeroboamu hakupata tena mamlaka* katika siku za Abiya; kisha Yehova akampiga, naye akafa.+
21 Lakini Abiya akaendelea kupata nguvu. Baada ya muda akaoa wake 14,+ akazaa wana 22 na mabinti 16. 22 Na mambo mengine katika historia ya Abiya, mambo aliyotenda na kusema, yameandikwa katika maandishi ya* nabii Ido.+
14 Kisha Abiya akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi;+ na Asa mwanawe akawa mfalme baada yake. Katika siku zake nchi ilikuwa na amani* kwa miaka kumi.
2 Asa alitenda yaliyokuwa mema na sawa machoni pa Yehova Mungu wake. 3 Aliondoa madhabahu za kigeni+ na mahali pa juu, akazivunjavunja nguzo takatifu,+ na kuikata miti mitakatifu.*+ 4 Zaidi ya hayo, aliwaambia watu wa Yuda wamtafute Yehova Mungu wa mababu zao na kushika Sheria na amri. 5 Kwa hiyo aliondoa mahali pa juu na vinara vya uvumba+ katika majiji yote ya Yuda, na chini ya utawala wake ufalme uliendelea kuwa bila usumbufu. 6 Alijenga majiji yenye ngome huko Yuda,+ kwa kuwa nchi haikuwa na usumbufu na hakuna yeyote aliyepigana vita naye katika miaka hiyo, kwa maana Yehova alimpumzisha.+ 7 Aliwaambia hivi watu wa Yuda: “Na tujenge majiji haya na kuyazingira kwa kuta na minara,+ malango* na makomeo. Kwa maana nchi bado imo mikononi mwetu kwa sababu tumemtafuta Yehova Mungu wetu. Tumemtafuta, naye ametupumzisha pande zote.” Kwa hiyo kazi yao ya ujenzi ilifanikiwa.+
8 Asa alikuwa na jeshi la wanaume 300,000 waliokuwa na ngao kubwa na mikuki. Na kutoka Benjamini kulikuwa na mashujaa hodari 280,000 waliobeba ngao ndogo* na kujihami kwa pinde.*+
9 Baadaye Zera Mwethiopia akaja kupigana nao akiwa na jeshi la wanaume 1,000,000 na magari 300 ya vita.+ Alipofika Maresha,+ 10 Asa akaenda kupigana naye, na Asa na jeshi lake wakajipanga kivita katika Bonde la Sefatha huko Maresha. 11 Kisha Asa akamlilia Yehova Mungu wake+ akisema: “Ee Yehova, haijalishi kwako ikiwa wale unaowasaidia ni wengi au hawana nguvu.+ Tusaidie, Ee Yehova Mungu wetu, kwa maana tunakutegemea* wewe,+ na katika jina lako tumekuja kupigana na umati huu.+ Ee Yehova, wewe ni Mungu wetu. Usiache mwanadamu anayeweza kufa akushinde.”+
12 Kwa hiyo Yehova akawashinda Waethiopia mbele ya Asa na mbele ya watu wa Yuda, na Waethiopia wakakimbia.+ 13 Asa na watu waliokuwa pamoja naye wakawafuatia mpaka Gerari,+ nao wakaendelea kuwaua Waethiopia hivi kwamba hakuna hata mmoja wao aliyebaki hai, kwa maana walipondwapondwa na Yehova na jeshi lake. Kisha wakachukua nyara nyingi sana. 14 Zaidi ya hayo, waliyashambulia majiji yote yaliyozunguka Gerari, kwa maana hofu ya Yehova ilikuwa imewashika wakaaji wa majiji hayo; nao wakapora majiji yote, kwa kuwa kulikuwa na vitu vingi vya kuporwa katika majiji hayo. 15 Walishambulia pia mahema ya wale waliokuwa na mifugo, wakateka idadi kubwa ya kondoo na ngamia, kisha wakarudi Yerusalemu.
15 Sasa roho ya Mungu ilimjia Azaria mwana wa Odedi. 2 Kwa hiyo akatoka kwenda kukutana na Asa, akamwambia: “Nisikilizeni, Asa na watu wote wa Yuda na Benjamini! Yehova yuko pamoja nanyi maadamu mnaendelea kuwa pamoja naye;+ nanyi mkimtafuta, atawaruhusu mumpate,+ lakini mkimwacha yeye atawaacha ninyi.+ 3 Kwa muda mrefu* Waisraeli hawakuwa na Mungu wa kweli, hawakuwa na kuhani wa kuwafundisha, na hawakuwa na sheria.+ 4 Lakini walipokuwa wakiteseka, walimrudia Yehova Mungu wa Israeli na kumtafuta, naye akawaruhusu wampate.+ 5 Siku hizo hakuna yeyote aliyeweza kusafiri akiwa salama,* kwa sababu kulikuwa na misukosuko mingi miongoni mwa wakaaji wote wa nchi mbalimbali. 6 Taifa lilikuwa likipondwa na taifa lingine na jiji likipondwa na jiji lingine, kwa sababu Mungu aliwavuruga kwa kila aina ya mateso.+ 7 Lakini ninyi, iweni imara na msivunjike moyo,*+ kwa maana mtapata thawabu kwa ajili ya kazi yenu.”
8 Mara tu Asa aliposikia maneno hayo na unabii wa nabii Odedi, akajipa ujasiri, akaondoa sanamu zenye kuchukiza katika nchi yote ya Yuda+ na Benjamini na katika majiji aliyokuwa ameteka katika eneo lenye milima la Efraimu, naye akajenga upya madhabahu ya Yehova iliyokuwa mbele ya ukumbi wa Yehova.+ 9 Akawakusanya pamoja watu wote wa Yuda na Benjamini na wakaaji wageni waliokuwa pamoja nao kutoka Efraimu na Manase na Simeoni,+ kwa maana walikuwa wamekimbia na kuja kwake kwa wingi kutoka Israeli walipoona kwamba Yehova Mungu wake alikuwa pamoja naye. 10 Basi wakakusanywa pamoja Yerusalemu katika mwezi wa tatu wa mwaka wa 15 wa utawala wa Asa. 11 Siku hiyo walimtolea Yehova dhabihu kutoka katika nyara walizoleta, ng’ombe 700 na kondoo 7,000. 12 Zaidi ya hayo, walifanya agano ili kumtafuta Yehova Mungu wa mababu zao kwa moyo wao wote na kwa nafsi* yao yote.+ 13 Mtu yeyote ambaye hangemtafuta Yehova Mungu wa Israeli angeuawa, awe mdogo au mkubwa, awe mwanamume au mwanamke.+ 14 Basi wakamwapia Yehova kwa sauti kubwa, kwa kelele za shangwe, na kwa tarumbeta na pembe. 15 Na watu wote wa Yuda wakashangilia kwa sababu ya kiapo hicho, kwa maana walikuwa wameapa kwa moyo wao wote, walimtafuta kwa bidii naye akawaruhusu wampate,+ na Yehova akaendelea kuwapumzisha pande zote.+
16 Mfalme Asa alimwondoa hata Maaka+ nyanya yake kutoka katika cheo chake cha mama malkia, kwa sababu alikuwa ametengeneza sanamu chafu sana* kwa ajili ya ibada ya mti mtakatifu.*+ Asa akaikatakata sanamu hiyo chafu sana, akaipondaponda na kuiteketeza katika Bonde la Kidroni.+ 17 Lakini mahali pa juu hapakuondolewa+ Israeli.+ Hata hivyo, moyo wa Asa ulikuwa kamili* maisha yake yote.*+ 18 Naye alileta katika nyumba ya Mungu wa kweli vitu ambavyo yeye na baba yake walikuwa wamevifanya kuwa vitakatifu—fedha, dhahabu, na vyombo mbalimbali.+ 19 Hakukuwa na vita mpaka mwaka wa 35 wa utawala wa Asa.+
16 Katika mwaka wa 36 wa utawala wa Asa, Mfalme Baasha+ wa Israeli alikuja kushambulia Yuda, akaanza kujenga* Rama+ ili kumzuia mtu yeyote asitoke wala kuingia kwa* Mfalme Asa wa Yuda.+ 2 Ndipo Asa akatoa fedha na dhahabu kutoka katika hazina za nyumba ya Yehova+ na nyumba ya* mfalme na kumpelekea Mfalme Ben-hadadi wa Siria,+ aliyekuwa akiishi Damasko, akamwambia: 3 “Kuna mkataba* kati yangu na wewe na kati ya baba yangu na baba yako. Ninakutumia fedha na dhahabu. Njoo, vunja mkataba wako* na Mfalme Baasha wa Israeli, ili aondoke kwangu.”
4 Ben-hadadi akamsikiliza Mfalme Asa, akawatuma wakuu wa majeshi yake kushambulia majiji ya Israeli, wakashinda Iyoni,+ Dani,+ Abel-maimu, na maghala yote ya majiji ya Naftali.+ 5 Baasha aliposikia habari hizo, mara moja akaacha kujenga* Rama, akasimamisha kazi hiyo. 6 Kisha Mfalme Asa akawachukua watu wote wa Yuda, nao wakabeba mawe na mbao zilizokuwa zikitumiwa na Baasha kujenga Rama,+ akazitumia kujenga* Geba+ na Mispa.+
7 Wakati huo mwonaji Hanani+ akaja kwa Mfalme Asa wa Yuda na kumwambia: “Kwa sababu ulimtegemea* mfalme wa Siria nawe hukumtegemea* Yehova Mungu wako, jeshi la mfalme wa Siria limeponyoka kutoka mikononi mwako.+ 8 Je, Waethiopia na Walibya hawakuwa jeshi kubwa sana lenye magari mengi ya vita na wapanda farasi? Lakini kwa sababu ulimtegemea Yehova, aliwatia mikononi mwako.+ 9 Kwa maana macho ya Yehova yanaenda huku na huku duniani kote+ ili adhihirishe nguvu zake* kwa niaba ya wale ambao moyo wao ni kamili* kumwelekea yeye.+ Umetenda kwa upumbavu katika jambo hili; kuanzia sasa na kuendelea kutakuwa na vita dhidi yako.”+
10 Hata hivyo, Asa akamkasirikia mwonaji huyo na kumtia gerezani,* alikasirishwa sana naye kwa sababu ya jambo hilo. Wakati huohuo, Asa akaanza kuwatesa watu wengine. 11 Sasa historia ya Asa, kuanzia mwanzo mpaka mwisho, imeandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na wa Israeli.+
12 Katika mwaka wa 39 wa utawala wake, Asa alishikwa na ugonjwa miguuni, akawa mgonjwa sana; na hata alipokuwa mgonjwa, hakumwomba Yehova msaada, bali waponyaji. 13 Kisha Asa akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake;+ alikufa katika mwaka wa 41 wa utawala wake. 14 Kwa hiyo walimzika katika kaburi lake la kifahari alilokuwa amejichimbia katika Jiji la Daudi;+ walimlaza kwenye machela ya kubebea maiti iliyojazwa mafuta ya zeri na mafuta* yaliyotengenezwa kwa njia ya pekee kwa mchanganyiko wa vikolezo mbalimbali.+ Isitoshe, waliwasha moto mkubwa isivyo kawaida kwa ajili yake.*
17 Na Yehoshafati+ mwanawe akawa mfalme baada yake, akaimarisha mamlaka yake juu ya Israeli. 2 Aliweka majeshi katika majiji yote ya Yuda yenye ngome na kuweka kambi za kijeshi katika nchi ya Yuda na katika majiji ya Efraimu ambayo Asa baba yake alikuwa ameyateka.+ 3 Yehova aliendelea kuwa pamoja na Yehoshafati kwa sababu alitembea katika njia za awali za Daudi babu yake+ naye hakutafuta Mabaali. 4 Kwa maana alimtafuta Mungu wa baba yake+ na kufuata* amri yake wala si mazoea ya Waisraeli.+ 5 Yehova aliendelea kuuimarisha kabisa ufalme mikononi mwake;+ na watu wote wa Yuda wakaendelea kumpa Yehoshafati zawadi, akawa na utajiri na utukufu mwingi.+ 6 Moyo wake ukawa jasiri katika njia za Yehova, na hata aliondoa mahali pa juu+ na miti mitakatifu*+ huko Yuda.
7 Katika mwaka wa tatu wa utawala wake aliwaita wakuu wake, yaani, Ben-haili, Obadia, Zekaria, Nethaneli, na Mikaya, ili wafundishe katika majiji ya Yuda. 8 Walikuwa pamoja na Walawi wafuatao: Shemaya, Nethania, Zebadia, Asaheli, Shemiramothi, Yehonathani, Adoniya, Tobaya, na Tob-adoniya, pamoja na kuhani Elishama na kuhani Yehoramu.+ 9 Walianza kufundisha nchini Yuda, wakiwa na kitabu cha Sheria ya Yehova,+ nao walizunguka katika majiji yote ya Yuda wakiwafundisha watu.
10 Na falme zote katika nchi zilizozunguka Yuda zikashikwa na hofu ya Yehova, nazo hazikumshambulia Yehoshafati. 11 Wafilisti wakamletea Yehoshafati zawadi na pesa kama ushuru. Waarabu wakamletea kondoo dume 7,700 na mbuzi dume 7,700 kutoka katika makundi yao.
12 Yehoshafati akaendelea kuwa mkuu zaidi na zaidi,+ akaendelea kujenga ngome+ na majiji yenye maghala+ huko Yuda. 13 Alitekeleza miradi mikubwa katika majiji ya Yuda, naye alikuwa na wanajeshi, mashujaa hodari, Yerusalemu. 14 Walipangwa kulingana na koo zao:* mkuu wa maelfu katika ukoo wa Yuda alikuwa mkuu Adna, naye alikuwa na mashujaa hodari 300,000.+ 15 Na mkuu Yehohanani alikuwa chini ya amri yake, naye alikuwa na mashujaa hodari 280,000. 16 Na pia Amasia mwana wa Zikri aliyejitolea kwa ajili ya utumishi wa Yehova alikuwa chini ya amri yake, naye alikuwa na mashujaa hodari 200,000. 17 Na kutoka katika ukoo wa Benjamini,+ kulikuwa na Eliada, shujaa hodari, naye alikuwa na wanaume 200,000 waliokuwa na pinde na ngao.+ 18 Na Yehozabadi alikuwa chini ya amri yake, naye alikuwa na wanaume 180,000 waliokuwa tayari kwa ajili ya vita. 19 Wanaume hao walikuwa wakimhudumia mfalme pamoja na wale ambao mfalme aliwaweka katika majiji yenye ngome kotekote nchini Yuda.+
18 Yehoshafati alikuwa na utajiri na utukufu mwingi,+ lakini alifanya mapatano ya ndoa pamoja na Ahabu.+ 2 Basi miaka kadhaa baadaye alishuka kwenda kwa Ahabu kule Samaria,+ na Ahabu akamtolea yeye na watu waliokuwa pamoja naye dhabihu ya kondoo na ng’ombe wengi. Naye akamhimiza* apande kwenda kushambulia Ramothi-gileadi.+ 3 Kisha Mfalme Ahabu wa Israeli akamuuliza Mfalme Yehoshafati wa Yuda: “Je, utaenda pamoja nami Ramothi-gileadi?” Akamjibu: “Mimi ni kama wewe, na watu wangu ni kama watu wako, nao watakuunga mkono vitani.”
4 Lakini Yehoshafati akamwambia mfalme wa Israeli: “Tafadhali, kwanza tafuta neno la Yehova.”+ 5 Kwa hiyo mfalme wa Israeli akawakusanya pamoja manabii, wanaume 400, akawauliza: “Je, twende kupigana vita dhidi ya Ramothi-gileadi, au nisiende?” Wakasema: “Panda uende, na Mungu wa kweli atalitia jiji hilo mikononi mwako mfalme.”
6 Kisha Yehoshafati akasema: “Je, hakuna nabii wa Yehova mahali hapa?+ Acheni tumuulize yeye pia.”+ 7 Ndipo mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati: “Bado kuna mtu mmoja+ ambaye tunaweza kumwomba ushauri kutoka kwa Yehova; lakini ninamchukia, kwa maana hatabiri kamwe mambo mema kunihusu, anatabiri mabaya sikuzote.+ Anaitwa Mikaya mwana wa Imla.” Hata hivyo, Yehoshafati akasema: “Mfalme, usiseme jambo kama hilo.”
8 Basi mfalme wa Israeli akamwita ofisa fulani wa makao ya mfalme na kumwambia: “Mlete haraka Mikaya mwana wa Imla.”+ 9 Sasa mfalme wa Israeli na Yehoshafati mfalme wa Yuda walikuwa wameketi kila mmoja wao kwenye kiti chake cha ufalme, akiwa amevaa mavazi ya kifalme, katika uwanja wa kupuria nafaka kwenye lango la kuingia Samaria, na manabii wote walikuwa wakitabiri mbele yao. 10 Kisha Sedekia mwana wa Kenaana akajitengenezea pembe za chuma na kusema: “Yehova anasema hivi: ‘Kwa pembe hizi utawapiga* Wasiria mpaka utakapowaangamiza.’” 11 Wale manabii wengine wote walikuwa wakitabiri vivyo hivyo, wakisema: “Panda mpaka Ramothi-gileadi, nawe utafanikiwa;+ Yehova atalitia jiji hilo mikononi mwako mfalme.”
12 Basi mjumbe aliyeenda kumwita Mikaya akamwambia: “Tazama! Manabii wote kwa pamoja wanasema mema kumhusu mfalme. Tafadhali, acha neno lako liwe kama maneno yao,+ useme mema.”+ 13 Lakini Mikaya akasema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, jambo lolote ambalo Mungu wangu atasema ndilo nitakalosema.”+ 14 Kisha akaingia kwa mfalme, naye mfalme akamuuliza: “Mikaya, je, twende kupigana vita dhidi ya Ramothi-gileadi, au nisiende?” Mara moja akajibu: “Panda uende nawe utafanikiwa; watatiwa mikononi mwako.” 15 Ndipo mfalme akamuuliza: “Nitakuapisha mara ngapi kwamba hupaswi kuniambia jambo lingine lolote isipokuwa ukweli katika jina la Yehova?” 16 Basi Mikaya akasema: “Ninawaona Waisraeli wote wakiwa wametawanyika milimani, kama kondoo wasio na mchungaji.+ Yehova akasema: ‘Hawa hawana bwana. Acha kila mmoja wao arudi kwa amani nyumbani kwake.’”
17 Kisha mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati: “Je, sikukwambia, ‘Hatatabiri mambo mema kunihusu, ila mabaya’?”+
18 Ndipo Mikaya akasema: “Basi, sikia neno la Yehova: Nilimwona Yehova akiwa ameketi kwenye kiti chake cha ufalme+ na jeshi lote la mbinguni+ likiwa limesimama upande wake wa kulia na upande wake wa kushoto.+ 19 Halafu Yehova akauliza, ‘Ni nani atakayemdanganya Mfalme Ahabu wa Israeli, ili apande kwenda na kufia huko Ramothi-gileadi?’ Na malaika mmoja akasema jambo moja na mwingine akasema jambo lingine. 20 Kisha roho*+ fulani akaja na kusimama mbele za Yehova na kusema, ‘Mimi nitamdanganya.’ Yehova akamuuliza, ‘Utatumia njia gani?’ 21 Akajibu, ‘Nitaenda na kuwa roho ya udanganyifu katika vinywa vya manabii wake wote.’ Kwa hiyo akasema, ‘Utamdanganya, na zaidi ya hilo, utafanikiwa. Nenda ukafanye hivyo.’ 22 Na sasa Yehova ametia roho ya udanganyifu katika vinywa vya hawa manabii wako,+ lakini Yehova ametangaza kwamba utapata msiba.”
23 Sasa Sedekia+ mwana wa Kenaana akamkaribia Mikaya+ na kumpiga kwenye shavu+ na kumuuliza: “Roho ya Yehova iliniacha jinsi gani na kuja kuzungumza nawe?”+ 24 Mikaya akamjibu: “Tazama! Utajua ni jinsi gani utakapoingia katika chumba cha ndani zaidi kujificha.” 25 Ndipo mfalme wa Israeli akasema: “Mchukue Mikaya umpeleke kwa Amoni mkuu wa jiji na kwa Yoashi mwana wa mfalme. 26 Waambie, ‘Mfalme anasema hivi: “Mfungeni mtu huyu gerezani+ na kumlisha kiasi kidogo cha mkate na maji mpaka nitakaporudi kwa amani.”’” 27 Lakini Mikaya akasema: “Ukirudi kwa amani, basi Yehova hajazungumza nami.”+ Kisha akasema: “Zingatieni maneno yangu, enyi watu wote.”
28 Basi mfalme wa Israeli na Yehoshafati mfalme wa Yuda wakapanda kwenda Ramothi-gileadi.+ 29 Ndipo mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati: “Nitabadili sura yangu na kuingia vitani, lakini wewe vaa mavazi yako ya kifalme.” Kwa hiyo mfalme wa Israeli akabadili sura yake, nao wakaingia vitani. 30 Sasa mfalme wa Siria alikuwa amewaagiza hivi makamanda wake wa magari ya vita: “Msipigane na yeyote, mdogo au mkubwa, isipokuwa mfalme wa Israeli.” 31 Na mara tu makamanda hao wa magari ya vita walipomwona Yehoshafati, wakaambiana: “Ni mfalme wa Israeli.” Basi wakamgeukia ili kupigana naye; na Yehoshafati akaanza kulilia msaada,+ na Yehova akamsaidia, na mara moja Mungu akawaelekeza upande mwingine ili wamwache. 32 Makamanda hao wa magari ya vita walipoona kwamba hakuwa mfalme wa Israeli, mara moja wakaacha kumfuatia.
33 Lakini mtu fulani alivuta upinde wake bila kukusudia* na kumpiga mfalme wa Israeli katikati ya sehemu ambazo koti lake la vita linaungana. Basi mfalme akamwambia mtu aliyeendesha gari lake: “Geuka uniondoe vitani,* kwa sababu nimejeruhiwa vibaya.”+ 34 Vita vikapamba moto siku hiyo yote, nao wakalazimika kumsimamisha mfalme ndani ya gari, akiwaelekea Wasiria mpaka jioni; akafa jua lilipokuwa likitua.+
19 Kisha Mfalme Yehoshafati wa Yuda akarudi salama salimini+ katika nyumba yake* huko Yerusalemu. 2 Yehu+ mwana wa mwonaji Hanani+ alienda kukutana na Mfalme Yehoshafati na kumuuliza: “Je, unapaswa kuwasaidia waovu,+ na je, unapaswa kuwapenda wale wanaomchukia Yehova?+ Kwa sababu hiyo ghadhabu ya Yehova iko dhidi yako. 3 Hata hivyo, kuna mambo mema ambayo yamepatikana ndani yako,+ kwa sababu uliiondoa kabisa miti mitakatifu* nchini, nawe umeutayarisha moyo wako* kumtafuta Mungu wa kweli.”+
4 Yehoshafati akaendelea kuishi Yerusalemu, naye akatoka tena na kwenda kukutana na watu kuanzia Beer-sheba mpaka kwenye eneo lenye milima la Efraimu,+ ili awarudishe kwa Yehova Mungu wa mababu zao.+ 5 Pia, aliwaweka waamuzi katika nchi yote, katika majiji yote ya Yuda yenye ngome, jiji baada ya jiji.+ 6 Akawaambia hivi waamuzi: “Iweni waangalifu kuhusu mambo mnayotenda, kwa maana hamhukumu kwa ajili ya mwanadamu bali kwa ajili ya Yehova, naye yupo pamoja nanyi mnapotoa hukumu.+ 7 Basi hofu ya Yehova na iwe juu yenu.+ Iweni waangalifu kuhusu mambo mnayotenda, kwa maana Yehova Mungu wetu hana ukosefu wa haki,+ hana ubaguzi,+ wala hapokei rushwa.”+
8 Pia huko Yerusalemu, Yehoshafati aliwaweka baadhi ya Walawi na makuhani na baadhi ya viongozi wa koo* za Waisraeli watumikie wakiwa waamuzi kwa ajili ya Yehova na kusuluhisha kesi za wakaaji wa Yerusalemu.+ 9 Akawaamuru: “Hivi ndivyo mnavyopaswa kufanya huku mkimwogopa Yehova, kwa uaminifu na kwa moyo kamili:* 10 Kila mara ndugu zenu wanaoishi katika majiji yao wakiwaletea kesi inayohusu umwagaji wa damu+ au swali kuhusu sheria fulani, amri, masharti, au maamuzi, mnapaswa kuwaonya ili wasiwe na hatia mbele za Yehova; msipofanya hivyo ghadhabu yake itakuja dhidi yenu na dhidi ya ndugu zenu. Hivyo ndivyo mnavyopaswa kufanya ili msiwe na hatia. 11 Ndiye huyu Amaria mkuu wa makuhani anayewasimamia katika kila jambo linalomhusu Yehova.+ Zebadia mwana wa Ishmaeli ndiye kiongozi wa ukoo wa Yuda katika kila jambo linalomhusu mfalme. Na Walawi watatumikia wakiwa maofisa wenu. Iweni imara, na mtende, na Yehova awe pamoja na wale wanaotenda mema.”*+
20 Baadaye Wamoabu+ na Waamoni,+ pamoja na baadhi ya Waamonimu,* wakaja kupigana vita na Yehoshafati. 2 Basi Yehoshafati akaambiwa hivi: “Umati mkubwa umekuja kukushambulia kutoka katika eneo la bahari,* kutoka Edomu,+ wamefika Hasason-tamari, yaani, En-gedi.”+ 3 Ndipo Yehoshafati akaogopa, akaazimia* kumtafuta Yehova.+ Basi akatangaza watu wote wa Yuda wafunge. 4 Kisha watu wa Yuda wakakusanyika pamoja kutafuta ushauri wa Yehova;+ walikuja kutoka katika majiji yote ya Yuda ili kutafuta ushauri wa Yehova.
5 Ndipo Yehoshafati akasimama katika kutaniko la Yuda na Yerusalemu ndani ya nyumba ya Yehova mbele ya ule ua mpya, 6 akasema:
“Ee Yehova Mungu wa mababu zetu, je, wewe si Mungu mbinguni;+ je, huna mamlaka juu ya falme zote za mataifa?+ Mkononi mwako mna nguvu na uwezo, na hakuna anayeweza kushindana nawe.+ 7 Ee Mungu wetu, je, hukuwafukuza wakaaji wa nchi hii kutoka mbele ya watu wako Waisraeli na kisha kuupa uzao wa* rafiki yako Abrahamu nchi hii iwe miliki yao ya kudumu?+ 8 Nao wakaishi katika nchi hiyo na kukujengea humo mahali patakatifu kwa ajili ya jina lako,+ wakisema, 9 ‘Tukipatwa na msiba, upanga, hukumu kali, au ugonjwa hatari, au njaa, na tusimame mbele ya nyumba hii na mbele zako (kwa maana jina lako limo katika nyumba hii)+ na kukulilia utusaidie katika taabu yetu, nawe usikie na kutuokoa.’+ 10 Sasa tazama, ndio hawa wanaume wa Amoni, Moabu, na eneo lenye milima la Seiri,+ ambao hukuwaruhusu Waisraeli wawavamie walipotoka nchini Misri. Waligeuka na kwenda mbali nao na hawakuwaangamiza.+ 11 Sasa wanatulipa kwa kuja kutufukuza kutoka katika miliki yako uliyotupatia iwe urithi wetu.+ 12 Ee Mungu wetu, je, hutatekeleza hukumu dhidi yao?+ Kwa maana hatuna nguvu mbele ya umati huu mkubwa unaokuja kutushambulia; nasi hatujui tunalopaswa kufanya,+ lakini macho yetu yanakutazama wewe.”+
13 Wakati huo, watu wote wa Yuda walikuwa wamesimama mbele za Yehova, pamoja na watoto wao wadogo, wake zao, na wana wao.
14 Ndipo katikati ya kutaniko, roho ya Yehova ikamjia Yahazieli mwana wa Zekaria mwana wa Benaya mwana wa Yeieli mwana wa Matania, Mlawi wa wana wa Asafu. 15 Akasema: “Sikilizeni kwa makini, enyi watu wote wa Yuda nanyi wakaaji wa Yerusalemu na Mfalme Yehoshafati! Yehova anawaambia hivi: ‘Msiogope wala msihofu kwa sababu ya umati huu mkubwa, kwa maana vita si vyenu bali ni vya Mungu.+ 16 Kesho shukeni kukabiliana nao. Watakuwa wakipanda kupitia njia ya Sisi, nanyi mtawakuta mwishoni mwa bonde* kabla ya nyika ya Yerueli. 17 Hamtahitaji kupigana vita hivi. Simameni mahali penu, simameni tuli,+ muuone wokovu wa Yehova kwa ajili yenu.*+ Enyi watu wa Yuda na Yerusalemu, msiogope wala msihofu.+ Kesho nendeni mkakabiliane nao, na Yehova atakuwa pamoja nanyi.’”+
18 Mara moja Yehoshafati akainama chini kifudifudi, na watu wote wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu wakaanguka chini mbele za Yehova ili kumwabudu Yehova. 19 Kisha Walawi waliokuwa wazao wa Wakohathi+ na wazao wa Wakora wakasimama ili kumsifu Yehova Mungu wa Israeli kwa sauti kubwa sana.+
20 Kesho yake, wakaamka asubuhi na mapema na kwenda katika nyika ya Tekoa.+ Walipokuwa wakienda, Yehoshafati akasimama na kusema: “Nisikilizeni, enyi watu wa Yuda nanyi wakaaji wa Yerusalemu! Iweni na imani katika Yehova Mungu wenu ili mweze kusimama imara.* Iweni na imani katika manabii wake,+ nanyi mtafanikiwa.”
21 Baada ya kushauriana na watu, aliwaweka wanaume ili wamwimbie+ Yehova na kumsifu wakiwa wamevaa mavazi matakatifu huku wakiwatangulia wanaume wenye silaha, wakisema: “Mshukuruni Yehova, kwa maana upendo wake mshikamanifu unadumu milele.”+
22 Walipoanza kuimba kwa shangwe nyimbo za sifa, Yehova akawaweka watu wawavizie wanaume wa Amoni, Moabu, na eneo lenye milima la Seiri waliokuwa wakivamia Yuda, nao wakaangamizana wenyewe kwa wenyewe.+ 23 Na Waamoni na Wamoabu wakageuka na kuwashambulia wakaaji wa eneo lenye milima la Seiri+ ili wawaue na kuwaangamiza kabisa; na baada ya kuwamaliza wakaaji wa Seiri, wakasaidiana kuangamizana wao kwa wao.+
24 Lakini watu wa Yuda walipofika kwenye mnara wa mlinzi wa nyikani+ na kutazama umati huo, waliona maiti zao zikiwa zimetapakaa ardhini;+ hakuna yeyote aliyeponyoka. 25 Basi Yehoshafati na watu wake wakaja kuchukua nyara kutoka kwao, wakapata vitu vingi sana, mavazi, na vitu vyenye kutamanika, ambavyo waliwavua mpaka waliposhindwa kubeba zaidi.+ Walichukua nyara hizo kwa siku tatu, kwa maana zilikuwa nyingi sana. 26 Siku ya nne walikusanyika pamoja katika Bonde la* Beraka, kwa maana walimsifu* Yehova huko. Ndiyo sababu tangu siku hiyo walipaita mahali hapo Bonde la Beraka.*+
27 Kisha watu wote wa Yuda na Yerusalemu, wakiongozwa na Yehoshafati, wakarudi Yerusalemu wakishangilia, kwa maana Yehova alikuwa amewafanya washangilie dhidi ya maadui wao.+ 28 Basi wakaingia Yerusalemu wakiwa na vinanda, vinubi,+ na tarumbeta+ na kwenda katika nyumba ya Yehova.+ 29 Na falme zote za nchi mbalimbali ziliposikia kwamba Yehova alikuwa amepigana na maadui wa Israeli zilishikwa na hofu ya Mungu.+ 30 Kwa hiyo ufalme wa Yehoshafati haukuwa na usumbufu wowote, na Mungu wake akaendelea kumpumzisha pande zote.+
31 Na Yehoshafati akaendelea kutawala Yuda. Alikuwa na umri wa miaka 35 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 25 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Azuba binti ya Shilhi.+ 32 Aliendelea kutembea katika njia ya Asa baba yake.+ Hakugeuka kutoka katika njia hiyo, naye alitenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova.+ 33 Hata hivyo, mahali pa juu hapakuondolewa,+ na bado watu hawakuwa wameutayarisha moyo wao kwa ajili ya Mungu wa mababu zao.+
34 Na mambo mengine katika historia ya Yehoshafati, kuanzia mwanzo mpaka mwisho, yameandikwa katika maandishi ya Yehu+ mwana wa Hanani,+ yaliyotiwa katika Kitabu cha Wafalme wa Israeli. 35 Baada ya hayo Mfalme Yehoshafati wa Yuda akaungana na Mfalme Ahazia wa Israeli, aliyetenda uovu.+ 36 Kwa hiyo akashirikiana naye katika kutengeneza meli za kwenda Tarshishi,+ walizitengenezea kule Esion-geberi.+ 37 Hata hivyo, Eliezeri mwana wa Dodavahu wa Maresha alitoa unabii dhidi ya Yehoshafati, akisema: “Kwa sababu umeungana na Ahazia, Yehova ataharibu kazi zako.”+ Basi meli hizo zikavunjika,+ kwa hiyo hazikuweza kwenda Tarshishi.
21 Kisha Yehoshafati akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi; na Yehoramu mwanawe akawa mfalme baada yake.+ 2 Ndugu zake, yaani, wana wa Yehoshafati, walikuwa Azaria, Yehieli, Zekaria, Azaria, Mikaeli, na Shefatia; hao wote walikuwa wana wa Mfalme Yehoshafati wa Israeli. 3 Na baba yao alikuwa amewapa zawadi nyingi za fedha na dhahabu, na vitu vyenye thamani, pamoja na majiji yenye ngome kule Yuda;+ lakini alimpa Yehoramu ufalme,+ kwa sababu yeye ndiye aliyekuwa mzaliwa wa kwanza.
4 Yehoramu alipochukua mamlaka ya ufalme wa baba yake, aliimarisha mamlaka yake kwa kuwaua ndugu zake wote+ kwa upanga, na pia baadhi ya wakuu wa Israeli. 5 Yehoramu alikuwa na umri wa miaka 32 alipoanza kutawala, naye alitawala huko Yerusalemu kwa miaka minane.+ 6 Alitembea katika njia ya wafalme wa Israeli,+ kama walivyofanya watu wa nyumba ya Ahabu, kwa maana alikuwa amemwoa binti ya Ahabu;+ na Yehoramu akaendelea kutenda maovu machoni pa Yehova. 7 Lakini Yehova hakutaka kuiangamiza nyumba ya Daudi kwa sababu ya agano alilokuwa amefanya pamoja na Daudi,+ kwa maana alikuwa ameahidi kumpa taa, yeye na wanawe, sikuzote.+
8 Katika siku zake, Waedomu waliasi nchi ya Yuda+ na kujichagulia mfalme wao wenyewe.+ 9 Basi Yehoramu na makamanda wake wakavuka na magari yake yote ya vita, naye akaondoka usiku na kuwashinda Waedomu waliokuwa wamemzingira yeye na makamanda wake wa magari ya vita. 10 Lakini tangu siku hiyo Waedomu wameendelea kuiasi nchi ya Yuda. Watu wa Libna+ pia walimwasi Yehoramu wakati huo, kwa sababu alikuwa amemwacha Yehova Mungu wa mababu zake.+ 11 Alikuwa amejenga pia mahali pa juu+ kwenye milima ya Yuda, akasababisha wakaaji wa Yerusalemu wafanye ukahaba wa kiroho, naye akawapotosha watu wa Yuda.
12 Baadaye alipokea barua kutoka kwa nabii Eliya+ iliyosema: “Yehova Mungu wa Daudi babu yako anasema, ‘Hujafuata* njia za Yehoshafati baba yako+ wala njia za Mfalme Asa+ wa Yuda. 13 Lakini unafuata njia ya wafalme wa Israeli+ na kusababisha watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu wafanye ukahaba wa kiroho+ kama ukahaba uliofanywa na nyumba ya Ahabu,+ na hata uliwaua ndugu zako mwenyewe,+ watu wa nyumba ya baba yako, waliokuwa bora kuliko wewe. 14 Kwa hiyo, Yehova anawaletea pigo kubwa watu wako, wana wako, wake zako, na mali zako zote. 15 Nawe utashikwa na magonjwa mengi, kutia ndani ugonjwa wa matumbo, mpaka ugonjwa huo utakaposababisha matumbo yako yatoke nje, siku baada ya siku.’”
16 Kisha Yehova akawachochea*+ Wafilisti+ na Waarabu+ walioishi karibu na Waethiopia ili wamshambulie Yehoramu. 17 Basi wakaivamia Yuda, wakaingia humo kwa nguvu na kuchukua mali zote zilizokuwa katika nyumba ya* mfalme,+ na pia wanawe na wake zake; Yehoahazi,*+ mwanawe wa mwisho, ndiye mwana pekee aliyebaki pamoja naye. 18 Na baada ya mambo hayo yote, Yehova akampiga kwa ugonjwa wa matumbo usioweza kupona.+ 19 Wakati fulani baadaye, baada ya miaka miwili kamili kupita, matumbo yake yalitoka nje kwa sababu ya ugonjwa huo, naye akafa alipokuwa akiteseka sana kwa sababu ya ugonjwa huo; na watu wake hawakuwasha moto kwa ajili yake kama ule uliowashwa kwa ajili ya mababu zake.+ 20 Alikuwa na umri wa miaka 32 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 8 huko Yerusalemu. Hakuna mtu yeyote aliyesikitishwa na kifo chake. Basi wakamzika katika Jiji la Daudi,+ lakini si katika makaburi ya wafalme.+
22 Kisha wakaaji wa Yerusalemu wakamweka Ahazia mwanawe wa mwisho kuwa mfalme baada yake, kwa maana kundi la wavamizi lililokuja kambini pamoja na Waarabu lilikuwa limewaua wana wote wakubwa wa Yehoramu.+ Kwa hiyo Ahazia mwana wa Yehoramu akaanza kutawala akiwa mfalme wa Yuda.+ 2 Ahazia alikuwa na umri wa miaka 22 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa mwaka mmoja huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Athalia+ mjukuu wa* Omri.+
3 Yeye pia alitembea katika njia za nyumba ya Ahabu,+ kwa maana mama yake alikuwa mshauri wake katika kutenda maovu. 4 Naye aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova, kama watu wa nyumba ya Ahabu, kwa maana walikuwa washauri wake baada ya kifo cha baba yake, jambo lililofanya aangamie. 5 Alifuata ushauri wao, akaenda pamoja na Yehoramu mwana wa Mfalme Ahabu wa Israeli kupigana vita na Mfalme Hazaeli+ wa Siria kule Ramothi-gileadi,+ ambako wapiga-mishale walimjeruhi Yehoramu. 6 Akarudi Yezreeli+ ili apone majeraha aliyopata kule Rama alipopigana na Mfalme Hazaeli wa Siria.+
Ahazia* mwana wa Yehoramu+ mfalme wa Yuda alishuka kwenda Yezreeli kumwona Yehoramu+ mwana wa Ahabu, kwa sababu alikuwa amejeruhiwa.*+ 7 Lakini Mungu alisababisha Ahazia aangamie alipokuja kwa Yehoramu; na alipokuja, alienda pamoja na Yehoramu kukutana na Yehu+ mjukuu* wa Nimshi, ambaye Yehova alikuwa amemtia mafuta ili awaangamize kabisa watu wa nyumba ya Ahabu.+ 8 Yehu alipoanza kutekeleza hukumu dhidi ya watu wa nyumba ya Ahabu, aliwapata wakuu wa Yuda na pia wana wa ndugu za Ahazia, wahudumu wa Ahazia, akawaua.+ 9 Kisha akamtafuta Ahazia; wakamkamata mahali alipokuwa akijificha kule Samaria na kumleta kwa Yehu. Halafu wakamuua na kumzika,+ kwa maana walisema: “Yeye ni mjukuu wa Yehoshafati, aliyemtafuta Yehova kwa moyo wake wote.”+ Hapakuwa na mtu yeyote wa nyumba ya Ahazia aliyekuwa na mamlaka ya kutawala ufalme huo.
10 Athalia,+ mama ya Ahazia, alipoona kwamba mwanawe amekufa, alitoka na kuangamiza uzao wote wa kifalme* wa nyumba ya Yuda.+ 11 Hata hivyo, Yehoshabeathi binti ya mfalme alimchukua Yehoashi+ mwana wa Ahazia, akamwiba kutoka miongoni mwa wana wa mfalme waliopaswa kuuawa na kumweka yeye pamoja na mlezi wake katika chumba cha ndani cha kulala. Yehoshabeathi binti ya Mfalme Yehoramu+ (alikuwa mke wa kuhani Yehoyada+ na dada ya Ahazia) alifanikiwa kumficha ili Athalia asimwone, kwa hiyo hakumuua.+ 12 Akakaa pamoja nao kwa miaka sita, akiwa amefichwa katika nyumba ya Mungu wa kweli Athalia alipokuwa akiitawala nchi.
23 Katika mwaka wa saba, Yehoyada alitenda kwa ujasiri na kufanya mapatano* na wakuu wa mamia,+ yaani, Azaria mwana wa Yerohamu, Ishmaeli mwana wa Yehohanani, Azaria mwana wa Obedi, Maaseya mwana wa Adaya, na Elishafati mwana wa Zikri. 2 Kisha wakazunguka katika nchi yote ya Yuda na kuwakusanya pamoja Walawi+ kutoka katika majiji yote ya Yuda na viongozi wa koo* za Waisraeli. Walipofika Yerusalemu, 3 kutaniko lote lilifanya agano+ pamoja na mfalme katika nyumba ya Mungu wa kweli, kisha akawaambia:
“Tazama! Mwana wa mfalme atatawala, kama Yehova alivyoahidi kuhusu wana wa Daudi.+ 4 Hivi ndivyo mtakavyofanya: Theluthi moja ya makuhani na ya Walawi watakaoshika zamu+ siku ya Sabato watalinda malango;+ 5 na theluthi nyingine watakuwa katika nyumba ya* mfalme,+ na theluthi nyingine watakuwa katika Lango la Msingi, na watu wote watakuwa katika nyua za nyumba ya Yehova.+ 6 Msimruhusu mtu yeyote aingie katika nyumba ya Yehova isipokuwa makuhani na Walawi wanaohudumu.+ Hao wanaweza kuingia kwa sababu ni kikundi kitakatifu, na watu wote watatimiza wajibu kwa Yehova. 7 Walawi wanapaswa kumzunguka mfalme pande zote, kila mmoja akiwa na silaha zake mikononi mwake. Yeyote atakayeingia katika nyumba hiyo atauawa. Mfuateni mfalme popote aendapo.”*
8 Walawi na watu wote wa Yuda wakafanya sawasawa na alivyoamuru kuhani Yehoyada. Basi kila mmoja wao akachukua wanaume wake waliokuwa na zamu siku ya Sabato, pamoja na wale ambao hawakuwa na zamu siku ya Sabato,+ kwa maana kuhani Yehoyada hakuwa ameviruhusu vikundi+ vilivyoshika zamu viondoke. 9 Kisha kuhani Yehoyada akawapa wakuu wa mamia+ mikuki na ngao ndogo* na ngao za mviringo zilizokuwa za Mfalme Daudi,+ ambazo zilikuwa katika nyumba ya Mungu wa kweli.+ 10 Halafu akawaweka watu wote, kila mmoja akiwa na silaha yake mkononi, kuanzia upande wa kulia wa nyumba mpaka upande wa kushoto wa nyumba, kando ya madhabahu na kando ya nyumba hiyo, kumzunguka mfalme pande zote. 11 Kisha wakamtoa nje mwana wa mfalme+ na kumvika taji na Ushahidi,*+ wakamweka kuwa mfalme, ndipo Yehoyada na wanawe wakamtia mafuta. Halafu wakasema: “Mfalme na aishi muda mrefu!”+
12 Athalia aliposikia sauti ya watu wakikimbia na kumsifu mfalme, mara moja akaja na kujiunga na watu katika nyumba ya Yehova.+ 13 Kisha akamwona mfalme akiwa amesimama hapo karibu na nguzo ya mfalme karibu na lango. Wakuu+ na wapiga tarumbeta walikuwa na mfalme, na watu wote nchini walikuwa wakishangilia+ na kupiga tarumbeta, na waimbaji wakiwa na ala za muziki waliongoza katika kutoa sifa.* Ndipo Athalia akayararua mavazi yake na kupaza sauti: “Ni njama! Ni njama!” 14 Lakini kuhani Yehoyada akawatoa nje wakuu wa mamia, wale waliowekwa kulisimamia jeshi, akawaambia: “Mwondoeni miongoni mwa vikosi, na yeyote akimfuata, muueni kwa upanga!” Kwa maana kuhani alikuwa amesema: “Msimuue ndani ya nyumba ya Yehova.” 15 Basi wakamkamata, na alipofika njia ya kuingia katika Lango la Farasi la nyumba ya* mfalme, mara moja wakamuua hapo.
16 Kisha Yehoyada akafanya agano kati yake na watu wote na mfalme, kwamba wataendelea kuwa watu wa Yehova.+ 17 Baada ya hayo, watu wote wakaenda kwenye nyumba ya Baali na kuibomoa,*+ wakavunja vipandevipande madhabahu zake na sanamu zake,+ nao wakamuua Matani kuhani wa Baali+ mbele ya madhabahu. 18 Kisha Yehoyada akaweka usimamizi wa nyumba ya Yehova mikononi mwa makuhani na Walawi, ambao Daudi alikuwa amewapanga katika vikundi wahudumu katika nyumba ya Yehova na kutoa dhabihu za kuteketezwa za Yehova+ kulingana na yale yaliyoandikwa katika Sheria ya Musa,+ wakishangilia na kuimba, kama alivyoagiza* Daudi. 19 Aliwaweka pia walinzi wa malango+ karibu na malango ya nyumba ya Yehova, ili mtu yeyote asiye safi kwa njia yoyote ile asiingie. 20 Kisha akawachukua wakuu wa mamia,+ watu mashuhuri, watawala wa watu, na watu wote nchini, wakamsindikiza mfalme kushuka kutoka katika nyumba ya Yehova. Halafu wakaja katika nyumba ya* mfalme kupitia lango la juu na kumweka mfalme kwenye kiti+ cha ufalme.+ 21 Basi watu wote nchini wakashangilia na jiji likatulia, kwa maana walikuwa wamemuua Athalia kwa upanga.
24 Yehoashi alikuwa na umri wa miaka saba alipoanza kutawala,+ naye alitawala kwa miaka 40 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Sibia kutoka Beer-sheba.+ 2 Yehoashi aliendelea kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova sikuzote za kuhani Yehoyada.+ 3 Yehoyada alimchagulia wake wawili, naye akazaa wana na mabinti.
4 Baadaye Yehoashi alitamani moyoni mwake kuirekebisha nyumba ya Yehova.+ 5 Kwa hiyo akawakusanya makuhani na Walawi na kuwaambia: “Nendeni kwenye majiji ya Yuda mkusanye kutoka kwa Waisraeli wote pesa za kurekebisha nyumba ya Mungu+ mwaka baada ya mwaka; nanyi mnapaswa kushughulikia jambo hili haraka.” Lakini Walawi hawakulishughulikia jambo hilo haraka.+ 6 Kwa hiyo, mfalme akamwita mkuu Yehoyada na kumuuliza:+ “Kwa nini hukuwaamuru Walawi walete kutoka Yuda na Yerusalemu kodi takatifu iliyoagizwa na Musa+ mtumishi wa Yehova, ile kodi takatifu ya kutaniko la Israeli, kwa ajili ya hema la Ushahidi?+ 7 Kwa maana wana wa Athalia,+ yule mwanamke mwovu, walikuwa wamevunja na kuingia ndani ya nyumba ya Mungu wa kweli,+ nao walikuwa wametumia vitu vyote vitakatifu vya nyumba ya Yehova kwa ajili ya Mabaali.” 8 Kisha, kwa agizo la mfalme, sanduku+ lilitengenezwa na kuwekwa nje kwenye lango la nyumba ya Yehova.+ 9 Halafu tangazo likatolewa katika nchi yote ya Yuda na Yerusalemu kwamba watu wamletee Yehova kodi takatifu+ ambayo Musa mtumishi wa Mungu wa kweli alikuwa amewaagiza Waisraeli nyikani. 10 Wakuu wote na watu wote wakashangilia,+ nao wakaendelea kuleta michango na kuitumbukiza katika sanduku hilo mpaka lilipojaa.*
11 Kila mara Walawi walipoleta sanduku hilo ili mfalme akabidhiwe, na maofisa walipoona kwamba kulikuwa na pesa nyingi ndani yake, mwandishi wa mfalme na mwakilishi wa kuhani mkuu walikuja na kuzitoa pesa sandukuni,+ kisha walilirudisha mahali pake. Hivyo ndivyo walivyofanya siku baada ya siku, nao walikusanya pesa nyingi. 12 Kisha mfalme pamoja na Yehoyada waliwapa wale waliosimamia kazi katika utumishi wa nyumba ya Yehova, na wasimamizi hao waliwaajiri watu waliokata mawe na mafundi wa kurekebisha nyumba ya Yehova,+ na pia mafundi wa chuma na shaba ili kuirekebisha nyumba ya Yehova. 13 Na wasimamizi hao wakaianzisha kazi, na kazi hiyo ya kurekebisha ikasonga mbele chini ya usimamizi wao, nao wakairudisha nyumba ya Mungu wa kweli katika hali yake inayofaa na kuiimarisha. 14 Na mara tu walipomaliza, walimletea mfalme na Yehoyada pesa zilizobaki, nao wakazitumia kutengeneza vyombo vya nyumba ya Yehova, vyombo vya huduma na vya kutolea dhabihu na vikombe na vyombo vya dhahabu na vya fedha.+ Nao walitoa kwa ukawaida dhabihu za kuteketezwa + katika nyumba ya Yehova sikuzote za Yehoyada.
15 Yehoyada alizeeka na kufa baada ya kuishi maisha marefu na yenye kuridhisha; alikuwa na umri wa miaka 130 alipokufa. 16 Basi wakamzika katika Jiji la Daudi pamoja na wafalme,+ kwa sababu alikuwa ametenda mema katika Israeli+ kwa ajili ya Mungu wa kweli na nyumba Yake.
17 Baada ya kifo cha Yehoyada, wakuu wa Yuda walikuja na kumwinamia mfalme, na mfalme akawasikiliza. 18 Waliiacha nyumba ya Yehova Mungu wa mababu zao na kuanza kuabudu miti mitakatifu* na sanamu, hivi kwamba hasira ya Mungu ikaja* dhidi ya Yuda na Yerusalemu kwa sababu ya hatia yao. 19 Aliendelea kuwatuma manabii miongoni mwao ili wawarudishe kwa Yehova, nao waliendelea kuwaonya* lakini walikataa kusikiliza.+
20 Roho ya Mungu ikamjia* Zekaria mwana wa kuhani Yehoyada,+ naye akasimama mahali palipo juu mbele ya watu na kuwaambia: “Mungu wa kweli anasema hivi: ‘Kwa nini mnazivunja amri za Yehova? Hamtafanikiwa! Kwa sababu mmemwacha Yehova, yeye naye, atawaacha ninyi.’”+ 21 Lakini walipanga njama dhidi yake,+ wakampiga mawe katika ua wa nyumba ya Yehova, kwa agizo la mfalme.+ 22 Kwa hiyo Mfalme Yehoashi hakukumbuka upendo mshikamanifu ambao Yehoyada baba yake* alimtendea, alimuua mwanawe, ambaye alisema hivi alipokuwa akifa: “Yehova na ashughulikie jambo hili na kukulipiza kisasi.”+
23 Mwanzoni mwa mwaka, jeshi la Siria lilikuja kumshambulia Yehoashi, likavamia Yuda na Yerusalemu.+ Kisha likawaua wakuu wote+ wa watu na kupeleka nyara zao zote kwa mfalme wa Damasko. 24 Kwa maana ingawa jeshi la Wasiria lililovamia lilikuwa na wanaume wachache, Yehova alitia mikononi mwao jeshi kubwa sana la watu wa Yuda na Yerusalemu+ kwa sababu walikuwa wamemwacha Yehova Mungu wa mababu zao; kwa hiyo wakatekeleza* hukumu dhidi ya Yehoashi. 25 Na walipoondoka katika nchi yake (kwa maana walimwacha akiwa amejeruhiwa vibaya*), watumishi wake mwenyewe walipanga njama dhidi yake kwa sababu alikuwa amemwaga damu ya wana* wa kuhani Yehoyada.+ Walimuua katika kitanda chake mwenyewe.+ Basi akafa na kuzikwa katika Jiji la Daudi,+ lakini hawakumzika katika makaburi ya wafalme.+
26 Hawa ndio waliopanga njama+ dhidi yake: Zabadi mwana wa Shimeathi mwanamke Mwamoni na Yehozabadi mwana wa Shimrithi mwanamke Mmoabu. 27 Na kuhusu wanawe na mambo mengi yaliyotangazwa dhidi yake+ na pia kazi ya kurekebisha* nyumba ya Mungu wa kweli,+ mambo hayo yote yameandikwa katika maandishi ya* Kitabu cha Wafalme. Na Amazia mwanawe akawa mfalme baada yake.
25 Amazia alikuwa na umri wa miaka 25 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 29 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Yehoadani wa Yerusalemu.+ 2 Aliendelea kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova, lakini si kwa moyo kamili. 3 Mara tu ufalme ulipoimarika kabisa mikononi mwake, aliwaua watumishi wake waliomuua mfalme, baba yake.+ 4 Lakini hakuwaua wana wao, kwa maana alitenda kulingana na mambo yaliyoandikwa katika Sheria, katika kitabu cha Musa, ambamo Yehova aliamuru hivi: “Akina baba hawapaswi kuuawa kwa sababu ya wana wao, na wana hawapaswi kuuawa kwa sababu ya baba zao; lakini kila mtu anapaswa kuuawa kwa sababu ya dhambi yake mwenyewe.”+
5 Na Amazia akawakusanya pamoja watu wa Yuda na kuwaagiza wasimame kulingana na koo zao,* chini ya wakuu wa maelfu na chini ya wakuu wa mamia kwa ajili ya watu wote wa Yuda na Benjamini.+ Akawaandikisha waliokuwa na umri wa miaka 20 na zaidi,+ akapata kwamba walikuwa mashujaa 300,000 waliozoezwa* kwa ajili ya utumishi wa kijeshi, walioweza kutumia mkuki na ngao kubwa. 6 Isitoshe, alikodi mashujaa hodari 100,000 kutoka Israeli kwa talanta 100 za fedha.* 7 Lakini mtu fulani wa Mungu wa kweli akamjia na kumwambia: “Ee mfalme, usiruhusu jeshi la Israeli liende pamoja nawe, kwa maana Yehova hayuko pamoja na Waisraeli,+ hayuko pamoja na Mwefraimu yeyote. 8 Lakini nenda peke yako, utende, na uwe jasiri vitani. Usipofanya hivyo, Mungu wa kweli anaweza kukufanya ujikwae mbele ya adui, kwa maana Mungu ana nguvu za kusaidia+ na za kusababisha mtu ajikwae.” 9 Ndipo Amazia akamuuliza hivi mtu wa Mungu wa kweli: “Lakini vipi kuhusu zile talanta 100 ambazo nimewapa wanajeshi wa Israeli?” Mtu wa Mungu wa kweli akamjibu: “Yehova anaweza kukupa nyingi zaidi kuliko hizo.”+ 10 Basi Amazia akawaagiza wanajeshi waliokuwa wamekuja kwake kutoka Efraimu waende zao, warudi kwao. Hata hivyo, waliwakasirikia sana watu wa Yuda, basi wakarudi kwao wakiwa wamekasirika sana.
11 Kisha Amazia akajipa ujasiri na kuwaongoza wanajeshi wake mwenyewe kwenye Bonde la Chumvi,+ akawaua wanaume 10,000 wa Seiri.+ 12 Na wanaume wa Yuda wakawateka watu 10,000 wakiwa hai. Wakawapandisha juu ya mwamba na kuwatupa chini kutoka kwenye mwamba huo, na wote wakavunjika vipandevipande. 13 Lakini wanajeshi ambao Amazia aliwaambia warudi, wasiende pamoja naye vitani,+ walikuwa wakivamia majiji ya Yuda, kuanzia Samaria+ mpaka Beth-horoni;+ waliwaua watu 3,000 katika majiji hayo na kuchukua nyara nyingi sana.
14 Lakini Amazia aliporudi baada ya kuwaua Waedomu, alileta miungu ya watu wa Seiri na kuisimamisha ili iwe miungu yake mwenyewe,+ naye akaanza kuinama mbele ya miungu hiyo na kuifukizia moshi wa dhabihu. 15 Kwa hiyo Yehova akamkasirikia sana Amazia, akamtuma nabii ambaye alimwambia: “Kwa nini unaifuata miungu ya mataifa ambayo haikuwaokoa watu wake kutoka mikononi mwako?”+ 16 Nabii huyo alipokuwa akizungumza naye, mfalme akamwambia: “Je, tulikuweka uwe mshauri wa mfalme?+ Nyamaza!+ Kwa nini unataka kuuawa?” Ndipo nabii huyo akanyamaza, lakini akasema: “Najua kwamba Mungu ameamua kukuangamiza, kwa sababu umetenda hivyo na hujasikiliza ushauri wangu.”+
17 Baada ya kushauriana na washauri wake, Mfalme Amazia wa Yuda alituma ujumbe kwa Yehoashi mwana wa Yehoahazi mwana wa Yehu mfalme wa Israeli akisema: “Njoo, tupambane vitani.”*+ 18 Mfalme Yehoashi wa Israeli akatuma ujumbe huu kwa Mfalme Amazia wa Yuda: “Gugu lenye miiba kule Lebanoni lilituma ujumbe huu kwa mwerezi huko Lebanoni, ‘Mpe mwanangu binti yako awe mke wake.’ Hata hivyo, mnyama wa mwituni wa Lebanoni akapita karibu na kulikanyaga-kanyaga gugu hilo lenye miiba. 19 Umesema, ‘Tazama! Nimewaangamiza Waedomu.’+ Kwa hiyo moyo wako umekuwa na kiburi, unataka utukuzwe. Lakini sasa kaa katika nyumba yako mwenyewe.* Kwa nini utafute msiba kisha uanguke, na kuwaangusha pia watu wa Yuda?”
20 Lakini Amazia hakusikiliza,+ kwa sababu Mungu wa kweli alikusudia kuwatia mikononi mwa adui,+ kwa sababu walikuwa wameifuata miungu ya Edomu.+ 21 Basi Mfalme Yehoashi wa Israeli akapanda kwenda huko, naye akapambana vitani na Mfalme Amazia wa Yuda huko Beth-shemeshi,+ jiji la Yuda. 22 Watu wa Yuda wakashindwa na Waisraeli, kwa hiyo kila mmoja akakimbilia nyumbani kwake.* 23 Mfalme Yehoashi wa Israeli akamkamata Mfalme Amazia wa Yuda, mwana wa Yehoashi mwana wa Yehoahazi,* huko Beth-shemeshi. Kisha akamleta Yerusalemu, naye akabomoa ukuta wa Yerusalemu kuanzia Lango la Efraimu+ mpaka Lango la Pembeni,+ urefu wa mikono 400.* 24 Akachukua dhahabu yote na fedha na vitu vyote vilivyokuwa katika nyumba ya Mungu wa kweli chini ya Obed-edomu na katika hazina za nyumba ya* mfalme,+ na pia akachukua mateka. Kisha akarudi Samaria.
25 Amazia+ mwana wa Yehoashi mfalme wa Yuda aliendelea kuishi kwa miaka 15 baada ya kifo cha Yehoashi+ mwana wa Yehoahazi mfalme wa Israeli.+ 26 Na mambo mengine katika historia ya Amazia, kuanzia mwanzo mpaka mwisho, je, hayajaandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na wa Israeli? 27 Kuanzia wakati ambapo Amazia aligeuka na kuacha kumfuata Yehova, walipanga njama+ dhidi yake huko Yerusalemu, akakimbilia Lakishi, lakini wakawatuma watu wamfuatie huko Lakishi, nao wakamuua huko. 28 Kwa hiyo wakambeba juu ya farasi na kumrudisha, wakamzika pamoja na mababu zake katika jiji la Yuda.
26 Kisha watu wote wa Yuda wakamchukua Uzia,+ aliyekuwa na umri wa miaka 16, wakamweka kuwa mfalme baada ya Amazia baba yake.+ 2 Alijenga upya jiji la Elothi+ na kulirudisha kwa Yuda baada ya mfalme* kuzikwa pamoja na mababu zake.+ 3 Uzia+ alikuwa na umri wa miaka 16 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 52 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Yekolia wa Yerusalemu.+ 4 Aliendelea kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova, kama Amazia baba yake alivyotenda.+ 5 Naye aliendelea kumtafuta Mungu katika siku za Zekaria, aliyemfundisha kumwogopa Mungu wa kweli. Wakati alipokuwa akimtafuta Yehova, Mungu wa kweli alimfanikisha.+
6 Alienda kupigana na Wafilisti+ na kuupenya ukuta wa Gathi,+ ukuta wa Yabne,+ na ukuta wa Ashdodi.+ Kisha akajenga majiji katika eneo la Ashdodi na miongoni mwa Wafilisti. 7 Mungu wa kweli aliendelea kumsaidia kuwashinda Wafilisti, Waarabu+ waliokuwa wakiishi Gurbaali, na Wameunimu. 8 Waamoni+ wakaanza kumpa Uzia ushuru. Hatimaye umaarufu wake ukaenea mpaka Misri, kwa maana alipata nguvu nyingi sana. 9 Isitoshe, Uzia alijenga minara+ Yerusalemu karibu na Lango la Pembeni,+ Lango la Bondeni,+ na Nguzo ya Kutegemeza Ukuta, naye akaiimarisha. 10 Pia, alijenga minara+ nyikani na kuchimba* matangi mengi ya maji (kwa maana alikuwa na mifugo mingi sana); alifanya hivyo pia katika Shefela na katika nchi tambarare ya juu. Alikuwa na wakulima na watunzaji wa mizabibu milimani na kule Karmeli, kwa maana alipenda kilimo.
11 Zaidi ya hayo, Uzia akawa na jeshi lililojihami kwa ajili ya vita. Wanajeshi hao walienda vitani, wakiwa wamepangwa katika vikundi. Walihesabiwa na kuandikishwa+ na mwandishi Yeieli+ na ofisa aliyeitwa Maaseya, chini ya amri ya Hanania, mmoja wa wakuu wa mfalme. 12 Idadi kamili ya viongozi wa koo* waliowaongoza mashujaa hao hodari ilikuwa 2,600. 13 Wanajeshi waliokuwa chini ya amri yao walikuwa 307,500, wanaume waliokuwa tayari kwa ajili ya vita, jeshi lenye nguvu la kumsaidia mfalme kupigana na maadui.+ 14 Uzia alilihami jeshi lote kwa ngao, mikuki,+ kofia, makoti ya vita,+ pinde, na mawe ya kombeo.+ 15 Pia, alitengeneza mitambo ya vita huko Yerusalemu iliyobuniwa na wahandisi; iliwekwa kwenye minara+ na kwenye pembe za kuta, nayo ilikuwa na uwezo wa kurusha mishale na mawe makubwa. Basi umaarufu wake ukaenea kwa mapana na marefu, kwa maana alisaidiwa sana akawa na nguvu.
16 Hata hivyo, mara tu alipokuwa na nguvu, moyo wake ukawa na kiburi ambacho kilisababisha aangamie, naye alikosa kutenda kwa uaminifu kumwelekea Yehova Mungu wake kwa kuwa aliingia katika hekalu la Yehova ili kufukiza uvumba kwenye madhabahu ya uvumba.+ 17 Mara moja kuhani Azaria na makuhani wengine 80 wa Yehova wenye ujasiri wakamfuata humo. 18 Wakamkabili Mfalme Uzia na kumwambia: “Si vyema kwako, Uzia, kumfukizia Yehova uvumba!+ Ni makuhani tu wanaopaswa kufukiza uvumba, kwa maana wao ni wazao wa Haruni,+ waliotakaswa. Toka mahali patakatifu, kwa maana hujatenda kwa uaminifu, na kwa sababu hiyo hutapokea utukufu wowote kutoka kwa Yehova Mungu.”
19 Lakini Uzia, aliyekuwa ameshika chetezo mkononi, akawaka hasira;+ na hasira yake ilipokuwa imewaka dhidi ya makuhani, ukoma+ ukatokea kwenye paji lake la uso mbele ya makuhani katika nyumba ya Yehova karibu na madhabahu ya uvumba. 20 Azaria mkuu wa makuhani na makuhani wote walipogeuka na kumtazama, waliona kwamba alikuwa amepigwa na ukoma kwenye paji la uso! Kwa hiyo wakamtoa humo haraka, naye mwenyewe akatoka nje haraka, kwa sababu Yehova alikuwa amemletea pigo.
21 Mfalme Uzia aliendelea kuwa na ukoma mpaka siku aliyokufa, naye aliendelea kukaa katika nyumba iliyotengwa akiwa mtu mwenye ukoma,+ kwa sababu alizuiwa kuingia katika nyumba ya Yehova. Yothamu mwanawe ndiye aliyesimamia nyumba ya* mfalme, akiwahukumu watu nchini.+
22 Na mambo mengine katika historia ya Uzia, kuanzia mwanzo mpaka mwisho, yaliandikwa na nabii Isaya+ mwana wa Amozi. 23 Kisha Uzia akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake, lakini alizikwa katika kiwanja cha kuzikia kilichokuwa mali ya wafalme, kwa maana walisema: “Ni mtu mwenye ukoma.” Na Yothamu mwanawe+ akawa mfalme baada yake.
27 Yothamu+ alikuwa na umri wa miaka 25 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 16 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Yerusha binti ya Sadoki.+ 2 Aliendelea kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova, kama alivyotenda Uzia baba yake,+ ila tu hakuingia kwa nguvu katika hekalu la Yehova.+ Lakini bado watu walikuwa wakitenda maovu. 3 Alijenga lango la juu la nyumba ya Yehova,+ naye alifanya kazi kubwa ya ujenzi kwenye ukuta wa Ofeli.+ 4 Alijenga pia majiji+ katika eneo lenye milima la Yuda,+ akajenga ngome+ na minara+ misituni. 5 Alipigana vita na mfalme wa Waamoni+ na hatimaye akawashinda, hivi kwamba mwaka huo Waamoni wakampa talanta 100 za fedha,* kori 10,000 za ngano,* na 10,000 za shayiri. Waamoni walimlipa vitu hivyo katika mwaka wa pili na wa tatu pia.+ 6 Basi Yothamu akaendelea kupata nguvu, kwa maana aliziimarisha* njia zake mbele za Yehova Mungu wake.
7 Na mambo mengine katika historia ya Yothamu, vita vyake vyote na njia zake, yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Israeli na wa Yuda.+ 8 Alikuwa na umri wa miaka 25 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 16 huko Yerusalemu.+ 9 Kisha Yothamu akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi.+ Na Ahazi mwanawe akawa mfalme baada yake.+
28 Ahazi+ alikuwa na umri wa miaka 20 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 16 huko Yerusalemu. Hakutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova kama alivyotenda Daudi babu yake.+ 2 Badala yake, alitembea katika njia za wafalme wa Israeli,+ na hata alitengeneza sanamu za chuma*+ za Mabaali. 3 Isitoshe, alifukiza moshi wa dhabihu katika Bonde la Mwana wa Hinomu* na kuwateketeza wanawe motoni,+ akifuata mazoea yenye kuchukiza ya mataifa+ ambayo Yehova alikuwa ameyafukuza kutoka mbele ya Waisraeli. 4 Aliendelea pia kutoa dhabihu na kufukiza moshi wa dhabihu mahali pa juu,+ kwenye vilima, na chini ya kila mti wenye majani mengi.+
5 Kwa hiyo Yehova Mungu wake akamtia mikononi mwa mfalme wa Siria,+ hivi kwamba wakamshinda, wakachukua mateka wengi, na kuwapeleka Damasko.+ Alitiwa pia mikononi mwa mfalme wa Israeli, ambaye aliwaua watu wake wengi. 6 Kwa maana Peka+ mwana wa Remalia aliwaua watu 120,000 huko Yuda katika siku moja, wote walikuwa wanaume jasiri, kwa sababu Waisraeli walikuwa wamemwacha Yehova Mungu wa mababu zao.+ 7 Na Zikri, shujaa Mwefraimu, alimuua Maaseya mwana wa mfalme na Azrikamu aliyekuwa msimamizi wa jumba la mfalme,* na Elkana aliyekuwa wa pili baada ya mfalme. 8 Zaidi ya hayo, Waisraeli waliwachukua mateka ndugu zao 200,000—wanawake, wana, na mabinti; walichukua pia nyara nyingi na kuzipeleka Samaria.+
9 Lakini nabii wa Yehova aliyeitwa Odedi alikuwa huko. Alienda kukutana na wanajeshi waliokuwa wakija Samaria na kuwaambia: “Tazameni! Yehova Mungu wa mababu zenu aliwatia watu wa Yuda mikononi mwenu kwa sababu walimkasirisha,+ nanyi mliwaua kwa hasira kali ambayo imefika mpaka mbinguni. 10 Na sasa mnakusudia kuwafanya watu wa Yuda na Yerusalemu wawe watumishi wenu wa kiume na wa kike.+ Lakini, je, ninyi pia hamna hatia mbele za Yehova Mungu wenu? 11 Sasa nisikilizeni, warudisheni ndugu zenu mliowachukua mateka, kwa maana hasira ya Yehova inayowaka iko dhidi yenu.”
12 Ndipo baadhi ya wakuu wa Waefraimu, Azaria mwana wa Yehohanani, Berekia mwana wa Meshilemothi, Yehizkia mwana wa Shalumu, na Amasa mwana wa Hadlai, wakawakabili watu waliokuwa wakitoka vitani, 13 wakawaambia: “Msiwalete mateka humu, kwa maana hilo litatufanya tuwe na hatia mbele za Yehova. Mnalokusudia kufanya litaongeza dhambi zetu na hatia yetu, kwa maana tayari tuna hatia kubwa na kuna hasira inayowaka dhidi ya Israeli.” 14 Basi wanajeshi hao wenye silaha wakawapa wakuu na kutaniko lote mateka na nyara+ walizochukua. 15 Kisha wanaume waliokuwa wamechaguliwa na kutajwa majina wakaenda na kuwachukua mateka, nao wakachukua mavazi kutoka katika zile nyara na kuwapa wote waliokuwa uchi. Basi wakawavika mavazi na kuwapa viatu, vyakula na vinywaji, na mafuta ya kujipaka. Zaidi ya hayo, waliwasafirisha kwa punda watu waliokuwa dhaifu na kuwapeleka kwa ndugu zao kule Yeriko, jiji la mitende. Kisha wakarudi Samaria.
16 Wakati huo Mfalme Ahazi aliwaomba wafalme wa Ashuru wamsaidie.+ 17 Na kwa mara nyingine tena Waedomu walivamia nchi ya Yuda, wakaishambulia na kuchukua mateka. 18 Wafilisti+ walivamia pia majiji ya Shefela+ na Negebu nchini Yuda na kuteka Beth-shemeshi,+ Aiyaloni,+ Gederothi, Soko na miji yake, Timna+ na miji yake, na Gimzo na miji yake; nao wakaanza kuishi humo. 19 Yehova aliwanyenyekeza watu wa Yuda kwa sababu ya Mfalme Ahazi wa Israeli, kwa maana aliwaacha watu wa Yuda watende watakavyo, na hivyo wakakosa kuwa waaminifu kwa Yehova kwa kiwango kikubwa.
20 Hatimaye Mfalme Tilgath-pilneseri+ wa Ashuru akaja kukabiliana naye na kumtesa+ badala ya kumtia nguvu. 21 Kwa maana Ahazi alikuwa amechukua kila kitu kilichokuwa katika nyumba ya Yehova na nyumba ya* mfalme+ na nyumba za wakuu na kumpa mfalme wa Ashuru kuwa zawadi; lakini hilo halikumsaidia kamwe. 22 Na wakati alipokuwa akiteseka, Mfalme Ahazi alikosa hata zaidi kuwa mwaminifu kwa Yehova. 23 Akaanza kuitolea dhabihu miungu ya Damasko+ iliyokuwa imemshinda,+ akasema: “Kwa sababu miungu ya wafalme wa Siria inawasaidia, nitaitolea dhabihu ili inisaidie.”+ Lakini miungu hiyo ilimfanya yeye na Waisraeli wote wajikwae. 24 Zaidi ya hayo, Ahazi alikusanya vyombo vya nyumba ya Mungu wa kweli; akavikata vipandevipande vyombo vya nyumba ya Mungu wa kweli,+ akaifunga milango ya nyumba ya Yehova,+ na kujitengenezea madhabahu katika kila pembe ya Yerusalemu. 25 Na katika majiji yote ya Yuda, alijenga mahali pa juu pa kuifukizia moshi wa dhabihu miungu mingine,+ akamkasirisha Yehova Mungu wa mababu zake.
26 Na mambo mengine katika historia yake, shughuli zake zote kuanzia mwanzo mpaka mwisho, yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na wa Israeli.+ 27 Kisha Ahazi akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake jijini Yerusalemu, kwa maana hawakumpeleka kwenye makaburi ya wafalme wa Israeli.+ Na Hezekia mwanawe akawa mfalme baada yake.
29 Hezekia+ alikuwa na umri wa miaka 25 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 29 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Abiya binti ya Zekaria.+ 2 Aliendelea kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova,+ kama alivyofanya Daudi babu yake.+ 3 Katika mwaka wa kwanza wa utawala wake, mwezi wa kwanza, aliifungua milango ya nyumba ya Yehova na kuirekebisha.+ 4 Kisha akawaleta makuhani na Walawi na kuwakusanya kwenye kiwanja kilichokuwa upande wa mashariki. 5 Akawaambia: “Nisikilizeni, enyi Walawi. Sasa jitakaseni+ na mwitakase nyumba ya Yehova Mungu wa mababu zenu, ondoeni kitu kichafu mahali patakatifu.+ 6 Kwa maana baba zetu wamekosa uaminifu nao wametenda maovu machoni pa Yehova Mungu wetu.+ Walimwacha na kugeuza nyuso zao mbali na hema la ibada la Yehova na kumgeuzia mgongo.+ 7 Pia, walifunga milango ya ukumbi+ na kuzima taa.+ Waliacha kufukiza uvumba+ na pia kumtolea Mungu wa Israeli dhabihu za kuteketezwa+ mahali patakatifu. 8 Kwa hiyo, ghadhabu ya Yehova ikaja dhidi ya watu wa Yuda na Yerusalemu,+ hivi kwamba akawafanya kuwa kitu cha kutisha na cha kushangaza na kitu cha kupigiwa mluzi,* kama mnavyoona kwa macho yenu wenyewe.+ 9 Kwa hiyo mababu zetu waliuawa kwa upanga,+ na wana wetu, mabinti wetu, na wake zetu wakapelekwa utekwani kwa sababu ya mambo hayo.+ 10 Sasa ninatamani moyoni mwangu kufanya agano pamoja na Yehova Mungu wa Israeli,+ ili hasira yake inayowaka ituondokee. 11 Wanangu, huu si wakati wa kupuuza mambo,* kwa maana Yehova amewachagua ninyi msimame mbele zake, muwe wahudumu wake,+ na kufukiza moshi wa dhabihu zake.”+
12 Ndipo Walawi wakasimama: Mahathi mwana wa Amasai na Yoeli mwana wa Azaria wa Wakohathi;+ kutoka kwa Wamerari,+ Kishi mwana wa Abdi na Azaria mwana wa Yehaleleli; kutoka kwa Wagershoni,+ Yoa mwana wa Zima na Edeni mwana wa Yoa; 13 kutoka kwa wana wa Elisafani, Shimri na Yeueli; kutoka kwa wana wa Asafu,+ Zekaria na Matania; 14 kutoka kwa wana wa Hemani,+ Yehieli na Shimei; kutoka kwa wana wa Yeduthuni,+ Shemaya na Uzieli. 15 Kisha wakawakusanya pamoja ndugu zao na kujitakasa, nao wakaja kama mfalme alivyoamuru kulingana na maneno ya Yehova, ili kuitakasa nyumba ya Yehova.+ 16 Ndipo makuhani wakaingia ndani ya nyumba ya Yehova ili kuitakasa, nao wakaondoa uchafu wote uliokuwa katika hekalu la Yehova na kuupeleka kwenye ua+ wa nyumba ya Yehova. Halafu Walawi wakauchukua na kuupeleka nje katika Bonde la Kidroni.+ 17 Kwa hiyo walianza kazi hiyo ya kutakasa katika siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, na katika siku ya nane ya mwezi huo wakafika katika ukumbi wa Yehova.+ Waliitakasa nyumba ya Yehova kwa siku nane, na katika siku ya 16 ya mwezi wa kwanza wakamaliza kazi hiyo.
18 Baada ya hayo wakaenda kwa Mfalme Hezekia na kumwambia: “Tumeitakasa nyumba yote ya Yehova, madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa+ na vyombo vyake vyote,+ na meza ya mikate ya tabaka*+ na vyombo vyake vyote. 19 Na vyombo vyote ambavyo Mfalme Ahazi aliviondoa wakati wa utawala wake alipokosa kutenda kwa uaminifu,+ tumevitayarisha na kuvitakasa,+ navyo viko mbele ya madhabahu ya Yehova.”
20 Basi Mfalme Hezekia akaamka mapema na kuwakusanya pamoja wakuu wa jiji, nao wakapanda kwenda katika nyumba ya Yehova. 21 Wakaleta ng’ombe dume saba, kondoo dume saba, wanakondoo dume saba, na mbuzi dume saba watolewe kuwa dhabihu ya dhambi kwa ajili ya ufalme, kwa ajili ya mahali patakatifu, na kwa ajili ya watu wa Yuda.+ Basi akawaambia makuhani, wazao wa Haruni, wawatoe dhabihu kwenye madhabahu ya Yehova. 22 Kisha wakawachinja ng’ombe hao,+ na makuhani wakachukua damu yao na kuinyunyiza kwenye madhabahu;+ halafu wakawachinja wale kondoo dume na kunyunyiza damu yao kwenye madhabahu, kisha wakawachinja wanakondoo dume hao na kunyunyiza damu yao kwenye madhabahu. 23 Kisha wakawaleta wale mbuzi dume wa dhabihu ya dhambi mbele ya mfalme na kutaniko na kuweka mikono yao juu yao. 24 Makuhani wakawachinja na kutoa dhabihu ya dhambi kwenye madhabahu wakitumia damu yao, ili kufunika dhambi za Waisraeli wote, kwa sababu mfalme alisema kwamba dhabihu ya kuteketezwa na dhabihu ya dhambi ilipaswa kutolewa kwa ajili ya Waisraeli wote.
25 Wakati huo, aliwaweka Walawi katika nyumba ya Yehova wakiwa na matoazi, vinanda, na vinubi,+ kulingana na amri ya Daudi+ na ya Gadi+ mwonaji wa mfalme na ya nabii Nathani,+ kwa maana amri hiyo ilitoka kwa Yehova kupitia manabii wake. 26 Basi Walawi walikuwa wakisimama wakiwa na ala za Daudi, na makuhani wakiwa na tarumbeta.+
27 Kisha Hezekia akaagiza dhabihu ya kuteketezwa itolewe kwenye madhabahu.+ Dhabihu ya kuteketezwa ilipoanza kutolewa, wimbo wa Yehova ulianza na pia milio ya tarumbeta, kwa kufuata mwongozo wa ala za Mfalme Daudi wa Israeli. 28 Na kutaniko lote likainama chini wimbo huo ulipokuwa ukiimbwa na tarumbeta kupigwa—yote hayo yaliendelea mpaka walipomaliza kutoa dhabihu ya kuteketezwa. 29 Na mara tu walipomaliza kutoa dhabihu hiyo, mfalme na wote waliokuwa pamoja naye wakainama chini na kusujudu. 30 Sasa Mfalme Hezekia na wakuu wakawaambia Walawi wamsifu Yehova kwa maneno ya Daudi+ na ya mwonaji Asafu.+ Kwa hiyo wakamsifu kwa shangwe nyingi, nao wakainama chini na kusujudu.
31 Kisha Hezekia akasema: “Sasa kwa kuwa mmetengwa kando* kwa ajili ya Yehova, njooni mlete dhabihu mbalimbali na dhabihu za shukrani katika nyumba ya Yehova.” Basi kutaniko likaanza kuleta dhabihu mbalimbali na dhabihu za shukrani, na kila mtu aliyekuwa na moyo wa kutoa kwa hiari alileta dhabihu za kuteketezwa.+ 32 Idadi ya dhabihu za kuteketezwa zilizoletwa na kutaniko ilikuwa ng’ombe 70, kondoo dume 100, wanakondoo dume 200—wote hao wakiwa dhabihu ya kuteketezwa kwa Yehova+— 33 na dhabihu takatifu zilikuwa ng’ombe 600 na kondoo 3,000. 34 Lakini hakukuwa na makuhani wa kutosha kuwachuna ngozi wanyama wote wa dhabihu za kuteketezwa, kwa hiyo ndugu zao Walawi waliwasaidia+ mpaka kazi hiyo ilipoisha na mpaka makuhani walipoweza kujitakasa,+ kwa kuwa Walawi walikuwa na bidii zaidi ya* kujitakasa kuliko makuhani. 35 Pia, kulikuwa na dhabihu nyingi za kuteketezwa,+ na vilevile vipande vya mafuta vya dhabihu za ushirika+ na matoleo ya vinywaji kwa ajili ya dhabihu za kuteketezwa.+ Hivyo utumishi wa nyumba ya Yehova ukaanzishwa tena.* 36 Kwa hiyo Hezekia na watu wote wakashangilia jambo ambalo Mungu wa kweli alikuwa amewafanyia watu,+ kwa sababu jambo hilo lilitendeka haraka sana.*
30 Hezekia akatuma ujumbe kwa watu wote wa Israeli+ na Yuda, na hata aliwaandikia barua watu wa Efraimu na Manase+ waje Yerusalemu katika nyumba ya Yehova kuadhimisha Pasaka ya Yehova Mungu wa Israeli.+ 2 Hata hivyo, mfalme, wakuu wake, na kutaniko lote Yerusalemu likaamua kuadhimisha Pasaka katika mwezi wa pili,+ 3 kwa maana hawakuweza kuiadhimisha wakati ambapo iliadhimishwa kwa ukawaida,+ kwa sababu hakukuwa na makuhani wa kutosha waliojitakasa+ na watu hawakuwa wamekusanyika Yerusalemu. 4 Mpango huo ulionekana kuwa mzuri machoni pa mfalme na kutaniko lote. 5 Basi wakaamua kutangaza kotekote Israeli, kuanzia Beer-sheba mpaka Dani,+ kwamba watu waje Yerusalemu kuadhimisha Pasaka ya Yehova Mungu wa Israeli, kwa maana wakiwa kikundi hawakuwa wameiadhimisha kulingana na yaliyoandikwa.+
6 Kisha wajumbe* wakaenda kotekote Israeli na Yuda wakiwa na barua hizo kutoka kwa mfalme na wakuu wake, kama mfalme alivyoamuru, akisema: “Watu wa Israeli, rudini kwa Yehova Mungu wa Abrahamu, Isaka, na Israeli, ili naye arudi kwa watu waliobaki walioponyoka kutoka mikononi mwa wafalme wa Ashuru.+ 7 Msiwe kama mababu zenu na kama ndugu zenu waliokosa kutenda kwa uaminifu kwa Yehova Mungu wa mababu zao, hivi kwamba akawafanya kuwa kitu cha kutisha, kama mnavyoona.+ 8 Sasa msiwe wakaidi kama mababu zenu.+ Jinyenyekezeni kwa Yehova, nanyi mje mahali pake patakatifu+ ambapo amepatakasa milele, mumtumikie Yehova Mungu wenu, ili hasira yake inayowaka iwaondokee.+ 9 Kwa maana mkirudi kwa Yehova, ndugu zenu na wana wenu wataonyeshwa rehema na wale waliowateka,+ nao wataruhusiwa kurudi katika nchi hii;+ kwa maana Yehova Mungu wenu ni mwenye huruma* na rehema,+ naye hataugeuza uso wake mbali nanyi mkirudi kwake.”+
10 Kwa hiyo wajumbe* hao walienda jiji hadi jiji katika nchi yote ya Efraimu na Manase,+ walifika hata Zabuloni, lakini watu walikuwa wakiwafanyia mzaha na kuwadhihaki.+ 11 Hata hivyo, watu fulani kutoka Asheri, Manase, na Zabuloni walijinyenyekeza na kuja Yerusalemu.+ 12 Mkono wa Mungu wa kweli ulikuwa pia juu ya watu wa Yuda ili kuwaunganisha* watekeleze yale ambayo mfalme na wakuu walikuwa wameamuru kulingana na neno la Yehova.
13 Umati wa watu ulikusanyika Yerusalemu katika mwezi wa pili+ kuadhimisha Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu;+ lilikuwa kutaniko kubwa sana. 14 Basi wakaondoa madhabahu zilizokuwa Yerusalemu,+ wakaziondoa madhabahu zote za kufukizia uvumba+ na kuzitupa katika Bonde la Kidroni. 15 Kisha wakamchinja mnyama wa Pasaka katika siku ya 14 ya mwezi wa pili. Makuhani na Walawi wakaona aibu, kwa hiyo wakajitakasa na kuleta dhabihu za kuteketezwa katika nyumba ya Yehova. 16 Nao wakasimama katika nafasi zao za kawaida, kulingana na Sheria ya Musa, mtu wa Mungu wa kweli; kisha makuhani wakanyunyiza damu+ waliyokabidhiwa na Walawi. 17 Kulikuwa na watu wengi katika kutaniko hilo ambao hawakuwa wamejitakasa, na Walawi ndio waliowachinja wanyama wa dhabihu za Pasaka kwa ajili ya wote ambao hawakuwa safi,+ ili wawatakase kwa Yehova. 18 Kwa maana idadi kubwa ya watu, hasa wale waliotoka Efraimu, Manase,+ Isakari, na Zabuloni, hawakuwa wamejitakasa, lakini bado walikula Pasaka, kinyume cha mambo yaliyoandikwa. Lakini Hezekia alisali kwa ajili yao, akisema: “Yehova, wewe uliye mwema,+ msamehe 19 kila mtu ambaye ameutayarisha moyo wake ili kukutafuta wewe Mungu wa kweli,+ Yehova, Mungu wa mababu zake, ingawa hajatakaswa kulingana na kiwango cha utakatifu.”+ 20 Basi Yehova akamsikiliza Hezekia, akawasamehe* watu hao.
21 Kwa hiyo Waisraeli waliokuwa Yerusalemu wakaadhimisha Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu+ kwa siku saba, wakiwa na shangwe nyingi,+ na Walawi na makuhani walikuwa wakimsifu Yehova siku baada ya siku, wakimpigia Yehova ala zao kwa sauti kubwa.+ 22 Zaidi ya hayo, Hezekia alizungumza na Walawi wote waliokuwa wakimtumikia Yehova kwa busara, akawatia moyo.* Nao wakala katika kipindi chote cha sherehe hiyo ya siku saba,+ wakitoa dhabihu za ushirika+ na kumshukuru Yehova Mungu wa mababu zao.
23 Kisha kutaniko lote likaamua kuendelea na sherehe hiyo kwa siku saba zaidi, kwa hiyo waliifanya kwa siku saba zaidi huku wakishangilia.+ 24 Na Mfalme Hezekia wa Yuda alitoa mchango wa ng’ombe dume 1,000 na kondoo 7,000 kwa ajili ya kutaniko, na wakuu walitoa mchango wa ng’ombe dume 1,000 na kondoo 10,000 kwa ajili ya kutaniko;+ na makuhani wengi walikuwa wakijitakasa.+ 25 Na kutaniko lote la Yuda, makuhani, Walawi, kutaniko lote lililotoka Israeli,+ na wakaaji wageni+ waliotoka katika nchi ya Israeli na wale walioishi Yuda wakaendelea kushangilia. 26 Na kulikuwa na shangwe nyingi Yerusalemu, kwa maana tangu siku za Sulemani mwana wa Daudi mfalme wa Israeli, jambo kama hilo halikuwa limeonekana Yerusalemu.+ 27 Hatimaye makuhani Walawi wakasimama na kuwabariki watu;+ na Mungu akasikia sauti yao, na sala yao ikafika katika makao yake matakatifu, mbinguni.
31 Mara tu walipomaliza kufanya mambo hayo yote, Waisraeli wote waliokuwepo wakaenda katika majiji ya Yuda, nao wakazivunjavunja nguzo takatifu,+ wakaikatakata miti mitakatifu,*+ na kubomoa mahali pa juu+ na madhabahu+ katika nchi yote ya Yuda na Benjamini, na pia kule Efraimu na Manase,+ mpaka walipoviharibu kabisa vitu hivyo, kisha Waisraeli wote wakarudi katika majiji yao, kila mmoja kwenye miliki yake.
2 Kisha Hezekia akawaweka makuhani katika vikundi vyao+ na Walawi katika vikundi vyao,+ kila kuhani na Mlawi katika utumishi wake,+ kwa ajili ya dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ushirika, ili wahudumu na kushukuru na kusifu katika malango ya nyua* za Yehova.+ 3 Baadhi ya mali za mfalme mwenyewe zilitolewa kwa ajili ya dhabihu za kuteketezwa,+ kutia ndani dhabihu zilizotolewa asubuhi na jioni,+ na pia dhabihu za kuteketezwa kwa ajili ya Sabato,+ miezi mipya,+ na sherehe mbalimbali,+ kulingana na mambo yaliyoandikwa katika Sheria ya Yehova.
4 Isitoshe, aliwaamuru watu walioishi Yerusalemu watoe fungu ambalo makuhani na Walawi walistahili kupokea,+ ili waishike kabisa* sheria ya Yehova. 5 Mara tu agizo hilo lilipotolewa, Waisraeli walitoa kwa wingi mazao ya kwanza ya nafaka, divai mpya, mafuta,+ na asali, na mazao yote ya shambani;+ walileta kwa wingi sehemu ya kumi ya kila kitu.+ 6 Na watu wa Israeli na wa Yuda waliokuwa wakiishi katika majiji ya Yuda walileta pia sehemu ya kumi ya ng’ombe na kondoo na sehemu ya kumi ya vitu vitakatifu+ vilivyotakaswa kwa ajili ya Yehova Mungu wao. Walivileta na kuvipanga katika marundo mengi. 7 Katika mwezi wa tatu,+ walianza kuvipanga katika marundo vitu walivyotoa michango; na katika mwezi wa saba+ wakamaliza. 8 Hezekia na wakuu walipokuja na kuona marundo hayo, walimsifu Yehova na kuwabariki watu wake Waisraeli.
9 Hezekia akawauliza makuhani na Walawi kuhusu marundo hayo, 10 ndipo Azaria mkuu wa makuhani wa nyumba ya Sadoki akamwambia: “Tangu watu walipoanza kuleta michango ndani ya nyumba ya Yehova,+ wamekuwa wakila na kushiba na bado kiasi kikubwa kimebaki, kwa maana Yehova amewabariki watu wake, na kiasi hiki kikubwa sana kimebaki.”+
11 Ndipo Hezekia akawaambia watayarishe vyumba vya kuhifadhia vitu hivyo*+ katika nyumba ya Yehova, basi wakavitayarisha. 12 Waliendelea kuleta kwa uaminifu michango, sehemu za kumi,+ na vitu vitakatifu; na Mlawi aliyeitwa Konania aliwekwa kuwa msimamizi wa vitu hivyo vyote, na Shimei ndugu yake alikuwa wa pili. 13 Yehieli, Azazia, Nahathi, Asaheli, Yerimothi, Yozabadi, Elieli, Ismakia, Mahathi, na Benaya walikuwa maofisa waliomsaidia Konania na Shimei ndugu yake, kama Mfalme Hezekia alivyoagiza, na Azaria alikuwa msimamizi wa nyumba ya Mungu wa kweli. 14 Na Kore mwana wa Imna, Mlawi aliyekuwa mlinzi wa malango upande wa mashariki,+ alisimamia matoleo ya hiari+ ya Mungu wa kweli, naye aligawa mchango uliotolewa kwa Yehova+ na pia vitu vitakatifu kabisa.+ 15 Na Edeni, Miniamini, Yeshua, Shemaya, Amaria, na Shekania walikuwa chini ya usimamizi wake katika majiji ya makuhani,+ katika wadhifa wao wa kuaminiwa, ili wawagawie ndugu zao kwa usawa katika vikundi,+ wakubwa kwa wadogo. 16 Hilo halikutia ndani mchango waliogawiwa wanaume wenye umri wa miaka mitatu na zaidi walioandikishwa kwenye orodha ya koo, ambao walikuja kila siku kutumikia katika nyumba ya Yehova na kutimiza majukumu ya vikundi vyao.
17 Makuhani waliandikishwa katika orodha ya koo kulingana na ukoo wao,*+ kama walivyoandikishwa Walawi waliokuwa na umri wa miaka 20 na zaidi,+ kulingana na majukumu ya vikundi vyao.+ 18 Walioandikishwa katika orodha ya koo walitia ndani watoto wao wote, wake zao, wana wao, na mabinti wao, kutaniko lote—kwa maana walidumisha utakaso wao kwa ajili ya mambo matakatifu kwa sababu ya wadhifa wao wa kuaminiwa— 19 na pia wazao wa Haruni, makuhani walioishi katika mashamba yenye malisho ambayo yalizunguka majiji yao.+ Katika majiji yote, wanaume walikuwa wamechaguliwa na kutajwa majina ili wampe mafungu kila mwanamume kuhani na kila mtu aliyeandikishwa katika orodha ya koo za Walawi.
20 Hezekia alifanya hayo katika nchi yote ya Yuda, naye aliendelea kutenda mema na yaliyo sawa na ya uaminifu mbele za Yehova Mungu wake. 21 Na kila kazi aliyofanya ili kumtafuta Mungu wake, iwe ni kuhusiana na utumishi wa nyumba ya Mungu wa kweli+ au kuhusiana na Sheria na amri, aliifanya kwa moyo wote, naye alifanikiwa.
32 Baada ya mambo hayo na matendo hayo ya uaminifu,+ Mfalme Senakeribu wa Ashuru alikuja na kuvamia Yuda. Alizingira majiji yenye ngome, akikusudia kuvunja na kuingia ndani na kuyateka.+
2 Hezekia alipoona kwamba Senakeribu amekuja akikusudia kulishambulia jiji la Yerusalemu, 3 alishauriana na wakuu wake na mashujaa wake na kuamua kuziba chemchemi za maji zilizokuwa nje ya jiji,+ nao wakamsaidia. 4 Watu wengi walikusanywa, nao wakaziba chemchemi zote na kijito kilichopita nchini, wakisema: “Kwa nini wafalme wa Ashuru waje na kupata maji mengi?”
5 Zaidi ya hayo, akiwa ameazimia, alijenga upya ukuta wote uliobomolewa, akajenga minara juu yake, na kujenga ukuta mwingine upande wa nje. Alirekebisha pia Kilima*+ cha Jiji la Daudi na kutengeneza silaha nyingi na ngao. 6 Kisha akawachagua wakuu wa majeshi wawaongoze watu, akawakusanya kwenye uwanja wa jiji uliokuwa karibu na lango la jiji, akawatia moyo* akisema: 7 “Iweni jasiri na imara. Msiogope wala msihofu kwa sababu ya mfalme wa Ashuru+ na umati wote ulio pamoja naye, kwa maana walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja naye.+ 8 Yeye anategemea mkono wa nyama* lakini sisi tuna Yehova Mungu wetu wa kutusaidia na kupigana vita vyetu.”+ Basi watu wakaimarishwa na maneno ya Mfalme Hezekia wa Yuda.+
9 Baada ya hayo, Mfalme Senakeribu wa Ashuru alipokuwa Lakishi+ pamoja na fahari yake yote ya kifalme,* aliwatuma watumishi wake Yerusalemu, kwa Mfalme Hezekia wa Yuda na kwa Wayudea wote waliokuwa Yerusalemu,+ akisema:
10 “Mfalme Senakeribu wa Ashuru anasema hivi: ‘Ni nini mnachotumainia kinachowafanya mkae Yerusalemu wakati limezingirwa?+ 11 Je, Hezekia hawapotoshi ili mfe kwa njaa kali na kiu, anaposema: “Yehova Mungu wetu atatuokoa kutoka mikononi mwa mfalme wa Ashuru”?+ 12 Je, siye Hezekia huyuhuyu aliyeondoa mahali pa juu+ pa Mungu wenu na madhabahu Zake+ kisha akawaambia watu wa Yuda na Yerusalemu: “Mnapaswa kuinama mbele ya madhabahu moja na kufukiza moshi wa dhabihu zenu”?+ 13 Je, hamjui yale ambayo mimi na mababu zangu tuliyatendea mataifa yote ya nchi mbalimbali?+ Je, miungu ya mataifa ya nchi hizo iliweza kuwaokoa kutoka mikononi mwangu?+ 14 Ni mungu gani kati ya miungu yote ya mataifa hayo ambayo mababu zangu waliiangamiza aliyeweza kuwaokoa watu wake kutoka mikononi mwangu, hivi kwamba Mungu wenu aweze kuwaokoa ninyi kutoka mikononi mwangu?+ 15 Sasa msiache Hezekia awadanganye au kuwapotosha hivyo!+ Msimwamini, kwa maana hakuna mungu yeyote wa taifa lolote au ufalme aliyeweza kuwaokoa watu wake kutoka mikononi mwangu na kutoka mikononi mwa mababu zangu. Basi, Mungu wenu atawezaje kuwaokoa ninyi kutoka mikononi mwangu?’”+
16 Watumishi wake wakasema mambo mengi zaidi mabaya dhidi ya Yehova Mungu wa kweli na dhidi ya Hezekia mtumishi wake. 17 Aliandika pia barua+ za kumtukana Yehova Mungu wa Israeli+ na kusema mambo mabaya dhidi yake, akisema: “Kama miungu ya mataifa ya nchi mbalimbali ilivyoshindwa kuwaokoa watu wake kutoka mikononi mwangu,+ vivyo hivyo Mungu wa Hezekia hatawaokoa watu wake kutoka mikononi mwangu.” 18 Waliendelea kuwaambia watu wa Yerusalemu waliokuwa ukutani mambo hayo kwa sauti kubwa kwa lugha ya Wayahudi, ili wawaogopeshe na kuwatia hofu, na ili waliteke jiji.+ 19 Walisema mambo mabaya dhidi ya Mungu wa Yerusalemu kama walivyosema dhidi ya miungu ya mataifa yaliyo duniani, ambayo ni kazi ya mikono ya mwanadamu. 20 Lakini Mfalme Hezekia na nabii Isaya+ mwana wa Amozi waliendelea kusali kuhusu jambo hilo na kuzililia mbingu ili wapate msaada.+
21 Ndipo Yehova akamtuma malaika, na malaika huyo akamwangamiza kabisa kila shujaa hodari,+ kiongozi, na mkuu katika kambi ya mfalme wa Ashuru, hivi kwamba akarudi katika nchi yake akiwa ameaibika. Baadaye aliingia katika nyumba ya* mungu wake, na humo baadhi ya wanawe mwenyewe wakamuua kwa upanga.+ 22 Basi Yehova akamwokoa Hezekia na wakaaji wa Yerusalemu kutoka mikononi mwa Mfalme Senakeribu wa Ashuru na kutoka mikononi mwa wengine wote na kuwapumzisha pande zote. 23 Na watu wengi wakamletea Yehova zawadi huko Yerusalemu na kumletea Mfalme Hezekia wa Yuda vitu bora,+ naye akaheshimiwa sana na mataifa yote baada ya mambo hayo.
24 Siku hizo Hezekia akawa mgonjwa karibu afe, akasali kwa Yehova,+ naye akamjibu na kumpa ishara.*+ 25 Lakini Hezekia hakuonyesha uthamini kwa wema wote aliotendewa, kwa maana moyo wake uliingiwa na kiburi, jambo lililomfanya yeye pamoja na watu wa Yuda na wa Yerusalemu wapatwe na ghadhabu. 26 Hata hivyo, Hezekia alijinyenyekeza, moyo wake ukaacha kuwa na kiburi,+ yeye pamoja na wakaaji wa Yerusalemu, na ghadhabu ya Yehova haikuja dhidi yao katika siku za Hezekia.+
27 Hezekia akapata utajiri mwingi sana na utukufu;+ akajijengea maghala+ ya kuweka fedha, dhahabu, mawe yenye thamani, mafuta ya zeri, ngao, na vitu vyote vyenye kutamanika. 28 Alijenga pia maghala ya mazao ya nafaka na divai mpya na mafuta, na pia mabanda kwa ajili ya mifugo ya kila aina na mabanda kwa ajili ya kondoo na mbuzi. 29 Pia alijijengea majiji, akapata mifugo mingi sana, makundi ya kondoo, mbuzi, na ng’ombe, kwa maana Mungu alimpa mali nyingi sana. 30 Hezekia ndiye aliyeziba chemchemi ya juu ya maji+ ya Gihoni+ na kuyaelekeza moja kwa moja chini upande wa magharibi katika Jiji la Daudi,+ na Hezekia alifanikiwa katika kila kazi aliyofanya. 31 Hata hivyo, wasemaji wa wakuu wa Babiloni walipotumwa wamuulize kuhusu ishara+ iliyokuwa imetokea* nchini,+ Mungu wa kweli alimwacha ili kumjaribu,+ ili ajue mambo yote yaliyokuwa moyoni mwake.+
32 Na mambo mengine katika historia ya Hezekia na matendo yake ya upendo mshikamanifu,+ yameandikwa katika maono ya nabii Isaya,+ mwana wa Amozi, katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na wa Israeli.+ 33 Kisha Hezekia akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake kwenye njia inayopanda kuelekea kwenye makaburi ya wana wa Daudi;+ na watu wote wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu wakamheshimu alipokufa. Na Manase mwanawe akawa mfalme baada yake.
33 Manase+ alikuwa na umri wa miaka 12 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 55 huko Yerusalemu.+
2 Alitenda maovu machoni pa Yehova, akafuata mazoea yenye kuchukiza ya mataifa ambayo Yehova alikuwa ameyafukuza kutoka mbele ya Waisraeli.+ 3 Alijenga upya mahali pa juu ambapo Hezekia baba yake alikuwa amebomoa,+ akajenga madhabahu kwa ajili ya Mabaali na kutengeneza miti mitakatifu,* naye akaliinamia jeshi lote la mbinguni na kuliabudu.+ 4 Alijenga pia madhabahu katika nyumba ya Yehova,+ ambayo Yehova alikuwa amesema hivi kuihusu: “Nitaweka jina langu Yerusalemu milele.”+ 5 Naye alijenga madhabahu kwa ajili ya jeshi lote la mbinguni katika nyua mbili za nyumba ya Yehova.+ 6 Na pia aliwateketeza* motoni wanawe mwenyewe+ katika Bonde la Mwana wa Hinomu;+ alifanya uchawi,+ alifanya uaguzi,* alifanya ulozi, na kuwaweka rasmi watu wanaowasiliana na roho na wabashiri.+ Alitenda kwa kiwango kikubwa sana mambo maovu machoni pa Yehova, na kumkasirisha.
7 Sanamu aliyokuwa amechonga aliiweka katika nyumba ya Mungu wa kweli+ ambayo Mungu alikuwa amemwambia hivi Daudi na Sulemani mwanawe kuihusu: “Nitaweka jina langu milele katika nyumba hii na katika jiji la Yerusalemu, ambalo nimelichagua kati ya makabila yote ya Israeli.+ 8 Ikiwa Waisraeli watashika kwa uangalifu mambo yote niliyowaamuru, Sheria yote, masharti na amri nilizowapa* kupitia Musa mtumishi wangu, sitaiondoa tena kamwe miguu yao katika nchi niliyowapa mababu zao.” 9 Manase aliendelea kuwapotosha watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu, akasababisha watende mambo maovu zaidi kuliko mataifa ambayo Yehova alikuwa ameyaangamiza kutoka mbele ya Waisraeli.+
10 Yehova aliendelea kuzungumza na Manase na watu wake, lakini hawakumsikiliza.+ 11 Kwa hiyo Yehova akawaleta wakuu wa jeshi la mfalme wa Ashuru ili wawashambulie, nao wakamkamata Manase kwa kulabu* na kumfunga kwa pingu mbili za shaba na kumpeleka Babiloni. 12 Alipokuwa akiteseka, alimsihi* Yehova Mungu wake amwonyeshe kibali, naye akaendelea kujinyenyekeza sana mbele za Mungu wa mababu zake. 13 Aliendelea kusali kwa Mungu, naye akaguswa na sala yake ya kusihi, akasikia ombi lake la kutaka kibali, akamrudisha Yerusalemu kwenye ufalme wake.+ Ndipo Manase akajua kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli.+
14 Baada ya hayo alijenga ukuta wa nje wa Jiji la Daudi+ upande wa magharibi wa Gihoni,+ bondeni,* na mpaka kwenye Lango la Samaki,+ akauzungusha hadi Ofeli,+ na kuufanya uwe mrefu sana. Zaidi ya hayo, aliwaweka wakuu wa jeshi katika majiji yote yenye ngome nchini Yuda. 15 Kisha akaondoa katika nyumba ya Yehova+ miungu ya kigeni na ile sanamu iliyochongwa na pia madhabahu zote alizokuwa amejenga kwenye mlima wa nyumba ya Yehova+ na Yerusalemu, akaagiza vitu hivyo vitupwe nje ya jiji. 16 Aliitayarisha pia madhabahu ya Yehova,+ akaanza kutoa juu yake dhabihu za ushirika+ na dhabihu za shukrani,+ naye akawaambia watu wa Yuda wamtumikie Yehova Mungu wa Israeli. 17 Hata hivyo, bado watu walikuwa wakitoa dhabihu mahali pa juu, ila tu sasa walimtolea Yehova Mungu wao.
18 Na mambo mengine katika historia ya Manase, sala aliyotoa kwa Mungu wake, na maneno ya waonaji waliozungumza naye katika jina la Yehova Mungu wa Israeli, yameandikwa katika historia ya wafalme wa Israeli. 19 Pia sala yake+ na jinsi ombi lake lilivyojibiwa, dhambi zake zote na jinsi alivyokosa kuwa mwaminifu,+ sehemu alizojenga mahali pa juu na kusimamisha miti mitakatifu*+ na sanamu za kuchongwa kabla hajajinyenyekeza, mambo hayo yameandikwa katika maandishi ya waonaji wake. 20 Kisha Manase akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake nyumbani kwake; na Amoni mwanawe akawa mfalme baada yake.+
21 Amoni+ alikuwa na umri wa miaka 22 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka miwili huko Yerusalemu.+ 22 Naye aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova, kama alivyofanya Manase baba yake;+ na Amoni akatoa dhabihu kwa sanamu zote za kuchongwa ambazo Manase baba yake alikuwa ametengeneza,+ naye akaendelea kuziabudu. 23 Lakini hakujinyenyekeza mbele za Yehova+ kama Manase baba yake alivyojinyenyekeza;+ badala yake, Amoni alizidisha sana hatia yake. 24 Hatimaye watumishi wake wakapanga njama dhidi yake+ na kumuua ndani ya nyumba yake mwenyewe. 25 Lakini watu wa nchi hiyo wakawaua wale wote waliopanga njama dhidi ya Mfalme Amoni,+ nao wakamweka Yosia mwanawe+ kuwa mfalme baada yake.
34 Yosia+ alikuwa na umri wa miaka minane alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 31 huko Yerusalemu.+ 2 Alitenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova na kutembea katika njia za Daudi babu yake, naye hakugeuka na kwenda kulia au kushoto.
3 Katika mwaka wa 8 wa utawala wake, alipokuwa angali mvulana, alianza kumtafuta Mungu wa Daudi babu yake;+ na katika mwaka wa 12, akaanza kusafisha Yuda na Yerusalemu+ kwa kuondoa mahali pa juu+ na miti mitakatifu,* sanamu za kuchongwa,+ na sanamu za chuma.* 4 Pia, walibomoa madhabahu za Mabaali mbele yake, naye akavikatakata vinara vya uvumba vilivyokuwa juu ya madhabahu hizo. Pia alivunja vipandevipande miti mitakatifu,* sanamu za kuchongwa, na sanamu za chuma,* akazipondaponda zikawa ungaunga na kuunyunyiza juu ya makaburi ya wale waliokuwa wakizitolea dhabihu.+ 5 Akaiteketeza mifupa ya makuhani juu ya madhabahu zao.+ Basi akaisafisha nchi ya Yuda na Yerusalemu.
6 Na katika majiji ya Manase, Efraimu,+ Simeoni, na mpaka Naftali, katika magofu yaliyozunguka majiji hayo, 7 alibomoa madhabahu na kupondaponda miti mitakatifu* na sanamu za kuchongwa,+ zikabaki ungaunga; naye akavikatakata vinara vyote vya uvumba katika nchi yote ya Israeli,+ kisha akarudi Yerusalemu.
8 Katika mwaka wa 18 wa utawala wake, alipokuwa ameisafisha nchi na hekalu,* alimtuma Shafani+ mwana wa Azalia, Maaseya mkuu wa jiji, na Yoa mwana wa Yoahazi aliyefanya kazi ya kuweka kumbukumbu ili wairekebishe nyumba ya Yehova Mungu wake.+ 9 Walienda kwa kuhani mkuu Hilkia na kumpa pesa zilizokuwa zimeletwa katika nyumba ya Mungu, ambazo Walawi waliokuwa walinzi wa malango walikuwa wamekusanya kutoka kwa watu wa kabila la Manase, Efraimu, na Waisraeli wengine wote,+ na pia kutoka kwa watu wa Yuda, Benjamini, na wakaaji wa Yerusalemu. 10 Kisha wakawapa pesa hizo wale waliowekwa kusimamia kazi katika nyumba ya Yehova. Halafu wafanyakazi waliokuwa katika nyumba ya Yehova wakazitumia kuikarabati na kuirekebisha nyumba hiyo. 11 Waliwapa mafundi na wajenzi ili wanunue mawe yaliyochongwa na mbao za kuunganisha na za kutengeneza maboriti ya kujenga nyumba ambazo wafalme wa Yuda waliacha ziharibike.+
12 Wanaume hao walifanya kazi hiyo kwa uaminifu.+ Walawi waliowekwa wawasimamie ni Yahathi na Obadia kutoka kwa Wamerari,+ na Zekaria na Meshulamu kutoka kwa Wakohathi,+ ili watumikie wakiwa waangalizi. Na Walawi fulani, ambao wote walikuwa wanamuziki stadi,+ 13 waliwasimamia vibarua* na walikuwa waangalizi wa watu wote waliokuwa wakifanya kazi katika utumishi wa aina mbalimbali; na baadhi ya Walawi walikuwa waandishi, maofisa, na walinzi wa malango.+
14 Walipokuwa wakitoa pesa zilizokuwa zimeletwa katika nyumba ya Yehova,+ kuhani Hilkia alipata kitabu cha Sheria ya Yehova+ kilichotolewa kupitia* Musa.+ 15 Kwa hiyo Hilkia akamwambia mwandishi Shafani: “Nimepata kitabu cha Sheria katika nyumba ya Yehova.” Basi Hilkia akampa Shafani kitabu hicho. 16 Kisha Shafani akampelekea mfalme kitabu hicho na kumwambia: “Watumishi wako wanafanya kila jambo ulilowaambia wafanye. 17 Wamekusanya* pesa zilizopatikana katika nyumba ya Yehova, nao wamewapa wanaume waliowekwa kusimamia kazi na wale wanaofanya kazi.” 18 Pia, mwandishi Shafani akamwambia mfalme: “Kuna kitabu ambacho kuhani Hilkia amenipa.”+ Kisha Shafani akaanza kukisoma mbele ya mfalme.+
19 Mara tu mfalme aliposikia maneno ya kitabu hicho cha Sheria, akayararua mavazi yake.+ 20 Kisha mfalme akamwagiza hivi Hilkia, Ahikamu+ mwana wa Shafani, Abdoni mwana wa Mika, mwandishi Shafani, na Asaya mtumishi wa mfalme: 21 “Nendeni mkatafute ushauri wa Yehova kwa niaba yangu na kwa niaba ya watu ambao wamebaki Israeli na Yuda kuhusu maneno ya kitabu hiki ambacho kimepatikana; kwa maana ghadhabu ya Yehova itakayomwagwa dhidi yetu ni kali kwa sababu mababu zetu hawakutekeleza neno la Yehova kwa kuyashika mambo yote yaliyoandikwa katika kitabu hiki.”+
22 Basi Hilkia, pamoja na wale waliotumwa na mfalme, wakaenda kwa nabii wa kike aliyeitwa Hulda.+ Alikuwa mke wa Shalumu mwana wa Tikva mwana wa Harhasi, mtunzaji wa chumba cha mavazi, naye alikuwa akiishi katika Wilaya ya Pili ya Yerusalemu; wakazungumza naye huko.+ 23 Akawaambia: “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Mwambieni hivi mtu aliyewatuma kwangu: 24 “Yehova anasema, ‘Nitaleta msiba mahali hapa na kwa wakaaji wake,+ laana zote zilizoandikwa katika kitabu+ walichosoma mbele ya mfalme wa Yuda. 25 Kwa sababu wameniacha+ na wanaifukizia miungu mingine moshi wa dhabihu ili kunikasirisha+ kwa kazi zote za mikono yao, ghadhabu yangu itamwagika mahali hapa nayo haitazimwa.’”+ 26 Lakini mwambieni hivi mfalme wa Yuda aliyewatuma kutafuta ushauri wa Yehova: “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Kuhusu maneno ambayo umesikia,+ 27 kwa sababu moyo wako ulikuwa msikivu,* nawe ukajinyenyekeza mbele za Mungu uliposikia mambo yake kuhusu mahali hapa na wakaaji wake, ukajinyenyekeza mbele zangu na kuyararua mavazi yako na kulia mbele zangu, mimi pia nimekusikia,+ asema Yehova. 28 Ndiyo sababu nitakuzika pamoja na mababu zako,* nawe utalazwa kwa amani katika kaburi lako, na macho yako hayataona msiba wote nitakaoleta mahali hapa na kwa wakaaji wake.’”’”+
Kisha wakampelekea mfalme jibu hilo. 29 Basi mfalme akatuma ujumbe na kuwakusanya wazee wote wa Yuda na Yerusalemu.+ 30 Baada ya hayo mfalme akapanda kwenda katika nyumba ya Yehova pamoja na wanaume wote wa Yuda, wakaaji wa Yerusalemu, makuhani, Walawi—watu wote, wadogo kwa wakubwa. Akasoma, watu wote wakisikia, maneno yote ya kitabu cha agano kilichokuwa kimepatikana katika nyumba ya Yehova.+ 31 Mfalme akasimama mahali pake na kufanya agano*+ mbele za Yehova, kwamba atamfuata Yehova na kushika amri zake, vikumbusho vyake, na masharti yake kwa moyo wake wote na kwa nafsi* yake yote+ kwa kutekeleza maneno ya agano hilo yaliyoandikwa katika kitabu hicho.+ 32 Zaidi ya hayo, aliwahimiza watu wote waliokuwa Yerusalemu na Benjamini wakubali agano hilo. Na wakaaji wa Yerusalemu wakatenda kulingana na agano la Mungu, Mungu wa mababu zao.+ 33 Kisha Yosia akaondoa vitu vyote vyenye kuchukiza* katika nchi zote za Waisraeli,+ naye akawafanya watu wote wa Israeli wamtumikie Yehova Mungu wao. Katika maisha yake yote* hawakuacha kumfuata Yehova Mungu wa mababu zao.
35 Yosia alifanya sherehe ya Pasaka+ ya Yehova huko Yerusalemu, nao wakamchinja mnyama wa Pasaka+ katika siku ya 14 ya mwezi wa kwanza.+ 2 Aliwaweka makuhani katika zamu zao na kuwatia moyo watekeleze utumishi wao wa nyumba ya Yehova.+ 3 Kisha akawaambia hivi Walawi, walimu wa Waisraeli wote,+ waliokuwa watakatifu kwa Yehova: “Liwekeni Sanduku takatifu ndani ya nyumba ambayo Sulemani mwana wa Daudi mfalme wa Israeli alijenga;+ hampaswi kulibeba tena mabegani mwenu.+ Sasa mtumikieni Yehova Mungu wenu na watu wake Waisraeli. 4 Na mjitayarishe kulingana na koo zenu,* kulingana na vikundi vyenu, mkifuata mambo yaliyoandikwa na Mfalme Daudi+ wa Israeli na Sulemani mwanawe.+ 5 Simameni mahali patakatifu mkiwa katika vikundi kulingana na koo* za ndugu zenu, ambao si Walawi,* pamoja na kikundi kinacholingana cha ukoo* wa Walawi. 6 Mchinjeni mnyama wa Pasaka+ na mjitakase na kufanya matayarisho kwa ajili ya ndugu zenu ili kutekeleza neno la Yehova kupitia Musa.”
7 Yosia akawachangia watu wote waliokuwepo makundi ya kondoo na mbuzi, wanakondoo dume na wanambuzi dume, kwa ajili ya dhabihu za Pasaka, jumla ya wanakondoo na wanambuzi 30,000, na pia ng’ombe 3,000. Wanyama hao walitolewa katika mali za mfalme mwenyewe.+ 8 Wakuu wake pia walitoa mchango uwe toleo la hiari kwa ajili ya watu, makuhani, na Walawi. Hilkia,+ Zekaria, na Yehieli, viongozi wa nyumba ya Mungu wa kweli, waliwapa makuhani wanyama 2,600 wa dhabihu za Pasaka na ng’ombe 300. 9 Konania na ndugu zake Shemaya na Nethaneli, pamoja na Hashabia, Yeieli, na Yozabadi, wakuu wa Walawi, waliwapa Walawi wanyama 5,000 wa dhabihu za Pasaka pamoja na ng’ombe 500 kuwa mchango.
10 Matayarisho ya utumishi huo yakafanywa, na makuhani wakasimama mahali pao na Walawi wakasimama kulingana na vikundi vyao,+ kama mfalme alivyokuwa ameamuru. 11 Wakawachinja wanyama wa Pasaka,+ na makuhani wakanyunyiza damu waliyopokea kutoka kwao,+ huku Walawi wakiwachuna ngozi wanyama hao.+ 12 Kisha wakatayarisha dhabihu za kuteketezwa ili kuwagawia watu wasio Walawi, ambao walikuwa wamepangwa kulingana na koo zao,* ili zitolewe kwa Yehova kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Musa; wakafanya vivyo hivyo kwa wale ng’ombe. 13 Waliipika* dhabihu ya Pasaka juu ya moto kulingana na desturi;+ nao wakapika matoleo matakatifu kwenye vyungu, sufuria kubwa, na vikaangio, kisha wakawaletea haraka watu wengine wote. 14 Kisha wakaitayarisha kwa ajili yao wenyewe na kwa ajili ya makuhani, kwa sababu makuhani, wazao wa Haruni, walikuwa wakitoa dhabihu za kuteketezwa na vipande vyenye mafuta mpaka giza lilipoingia, kwa hiyo Walawi wakaitayarisha kwa ajili yao wenyewe na kwa ajili ya makuhani, wazao wa Haruni.
15 Na waimbaji, wana wa Asafu,+ walisimama mahali pao kama alivyoamuru Daudi,+ Asafu,+ Hemani, na Yeduthuni,+ mwonaji wa mfalme; na walinzi wa malango walikuwa kwenye malango mbalimbali.+ Hawakuhitaji kuacha utumishi wao, kwa sababu ndugu zao Walawi walikuwa wamewatayarishia Pasaka. 16 Kwa hiyo utumishi wote wa Yehova ukatayarishwa siku hiyo ili kuadhimisha Pasaka+ na kutoa dhabihu za kuteketezwa kwenye madhabahu ya Yehova, kulingana na agizo la Mfalme Yosia.+
17 Waisraeli waliokuwepo waliadhimisha Pasaka wakati huo na pia Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu kwa siku saba.+ 18 Pasaka kama hiyo haikuwa imewahi kuadhimishwa Israeli tangu siku za nabii Samweli; wala wafalme wengine wa Israeli hawakuwa wameadhimisha Pasaka kama hiyo iliyoadhimishwa na Yosia,+ makuhani, Walawi, watu wote wa Yuda na Israeli waliokuwepo, na wakaaji wa Yerusalemu. 19 Pasaka hii ilifanywa katika mwaka wa 18 wa utawala wa Yosia.
20 Baada ya hayo yote, Yosia alipokuwa ametayarisha hekalu,* Mfalme Neko+ wa Misri alipanda kuja kupigana Karkemishi karibu na Mto Efrati. Kisha Yosia akaenda kukabiliana naye.+ 21 Kwa hiyo akamtumia Yosia wajumbe, akisema: “Vita hivi vinakuhusuje, Ee mfalme wa Yuda? Sijaja kupigana nawe leo, nimekuja kupigana na nyumba nyingine, na Mungu anasema kwamba ninapaswa kufanya haraka. Kwa faida yako mwenyewe, acha kumpinga Mungu, aliye pamoja nami, la sivyo atakuangamiza.” 22 Hata hivyo, Yosia hakugeuka na kumwacha, lakini alibadili sura yake+ ili apigane naye, akakataa kabisa kusikiliza maneno ya Neko, yaliyotoka kinywani mwa Mungu. Basi akaja kupigana naye katika Nchi Tambarare ya Megido.+
23 Na wapiga mishale wakampiga Mfalme Yosia, akawaambia watumishi wake: “Niondoeni hapa, kwa maana nimejeruhiwa vibaya sana.” 24 Kwa hiyo watumishi wake wakamtoa garini, wakamweka kwenye gari lake la pili la vita na kumpeleka Yerusalemu. Kwa hiyo akafa na kuzikwa katika kaburi la mababu zake,+ na watu wote wa Yuda na Yerusalemu wakamwombolezea Yosia. 25 Na Yeremia+ akamwimbia Yosia wimbo wa maombolezo, na tangu siku hiyo waimbaji wote wa kiume na wa kike+ wanaendelea kuimba kumhusu Yosia katika nyimbo zao za huzuni;* na uamuzi ukafanywa kwamba nyimbo hizo zinapaswa kuimbwa katika nchi ya Israeli, nazo zimeandikwa katika nyimbo za huzuni.
26 Na mambo mengine katika historia ya Yosia na matendo yake ya upendo mshikamanifu, kulingana na mambo yaliyoandikwa katika Sheria ya Yehova, 27 na mambo aliyofanya, kuanzia mwanzo mpaka mwisho, yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Israeli na wa Yuda.+
36 Kisha watu nchini wakamchukua Yehoahazi+ mwana wa Yosia na kumweka kuwa mfalme huko Yerusalemu baada ya baba yake.+ 2 Yehoahazi alikuwa na umri wa miaka 23 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miezi mitatu huko Yerusalemu. 3 Hata hivyo, mfalme wa Misri akamwondoa madarakani huko Yerusalemu na kuitoza nchi talanta 100 za fedha * na talanta moja ya dhahabu.+ 4 Zaidi ya hayo, mfalme wa Misri alimweka Eliakimu ndugu ya Yehoahazi kuwa mfalme wa Yuda na Yerusalemu na kubadili jina lake kuwa Yehoyakimu; lakini Neko+ akamchukua Yehoahazi ndugu yake na kumpeleka Misri.+
5 Yehoyakimu+ alikuwa na umri wa miaka 25 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 11 huko Yerusalemu. Aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova Mungu wake.+ 6 Mfalme Nebukadneza+ wa Babiloni alipanda kuja kumshambulia, akamfunga kwa pingu mbili za shaba na kumpeleka Babiloni.+ 7 Pia Nebukadneza alichukua baadhi ya vyombo vya nyumba ya Yehova, akavipeleka Babiloni na kuviweka katika jumba lake la kifalme huko Babiloni.+ 8 Na mambo mengine katika historia ya Yehoyakimu, mambo yenye kuchukiza aliyotenda na mambo yasiyofaa yaliyopatikana dhidi yake, yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Israeli na wa Yuda; na Yehoyakini mwanawe akawa mfalme baada yake.+
9 Yehoyakini+ alikuwa na umri wa miaka 18 alipoanza kutawala, alitawala kwa miezi mitatu na siku kumi huko Yerusalemu; naye aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova.+ 10 Mwanzoni mwa mwaka,* Mfalme Nebukadneza aliagiza aletwe Babiloni,+ pamoja na vyombo vyenye thamani vya nyumba ya Yehova.+ Akamweka Sedekia ndugu ya baba yake kuwa mfalme wa Yuda na Yerusalemu.+
11 Sedekia+ alikuwa na umri wa miaka 21 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 11 huko Yerusalemu.+ 12 Aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova Mungu wake. Hakujinyenyekeza mbele ya nabii Yeremia,+ aliyesema mambo aliyoagizwa na Yehova. 13 Pia alimwasi Mfalme Nebukadneza,+ aliyekuwa amemwapisha kwa jina la Mungu, akaendelea kuwa mkaidi* na mwenye moyo mgumu na kukataa kumgeukia Yehova Mungu wa Israeli. 14 Wakuu wote wa makuhani na pia watu walikosa uaminifu kupita kiasi, wakitenda mambo yote yenye kuchukiza ya mataifa, nao wakaichafua nyumba ya Yehova+ aliyokuwa ameitakasa Yerusalemu.
15 Yehova Mungu wa mababu zao aliendelea kuwaonya kupitia wajumbe wake, aliwaonya tena na tena, kwa sababu aliwahurumia watu wake na makao yake. 16 Lakini waliendelea kuwadhihaki wajumbe wa Mungu wa kweli,+ wakadharau maneno yake+ na kuwakejeli manabii wake,+ mpaka ghadhabu ya Yehova ilipokuja dhidi ya watu wake,+ hivi kwamba hawangeweza kuponywa.
17 Kwa hiyo akamleta mfalme wa Wakaldayo awashambulie,+ ambaye aliwaua wanaume wao vijana kwa upanga+ katika nyumba ya mahali pao patakatifu;+ hakumhurumia kijana wa kiume wala bikira, mzee wala aliye dhaifu.+ Mungu alitia kila kitu mikononi mwake.+ 18 Alipeleka kila kitu Babiloni, vyombo vyote vya nyumba ya Mungu wa kweli, vikubwa na vidogo, na pia hazina za nyumba ya Yehova na hazina za mfalme na wakuu wake.+ 19 Aliiteketeza kabisa nyumba ya Mungu wa kweli,+ akaubomoa ukuta wa Yerusalemu,+ akateketeza kwa moto minara yake yote yenye ngome, na kuharibu kila kitu chenye thamani.+ 20 Aliwachukua mateka na kuwapeleka Babiloni wale ambao hawakuuawa kwa upanga,+ nao wakawa watumishi wake+ na wa wanawe mpaka ufalme wa Uajemi ulipoanza kutawala,+ 21 ili kutimiza neno la Yehova lililosemwa na Yeremia,+ mpaka nchi ilipolipa sabato zake.+ Sikuzote ilipokuwa ukiwa ilishika sabato, ili kutimiza miaka 70.+
22 Katika mwaka wa kwanza wa utawala wa Mfalme Koreshi+ wa Uajemi, ili neno la Yehova lililosemwa na Yeremia+ litimie, Yehova aliichochea roho ya Mfalme Koreshi wa Uajemi atoe tangazo katika ufalme wake wote, ambalo pia aliliandika,+ akisema: 23 “Mfalme Koreshi wa Uajemi anasema hivi: ‘Yehova Mungu wa mbinguni amenipa falme zote za dunia,+ naye ameniagiza nimjengee nyumba Yerusalemu, nchini Yuda.+ Yeyote miongoni mwenu, ninyi watu wake wote, Yehova Mungu wake na awe pamoja naye, na apande kwenda huko.’”+
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Au “walikuwa wakitafuta ushauri Wake hapo.”
Tnn., “nitoke nje mbele ya watu hawa na kurudi ndani.”
Tnn., “siku nyingi.”
Au “wapanda farasi.”
Au “wapanda farasi.”
Au labda, “kutoka Misri na kutoka Kue; wafanyabiashara wa mfalme waliwanunua kutoka Kue,” huenda ni Kilikia.
Au “jumba la mfalme.”
Au “wabeba mizigo.”
Au “jumba la mfalme la.”
Yaani, mikate ya wonyesho.
Kori moja ilikuwa sawa na lita 220 (kilogramu 170 hivi). Angalia Nyongeza B14.
Bathi ilikuwa sawa na lita 22. Angalia Nyongeza B14.
Au “wabeba mizigo.”
Kipimo cha kawaida cha mkono mmoja kililingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5), lakini baadhi ya watu wanahisi kwamba “kipimo cha awali” kinarejelea kipimo cha mkono mrefu ambacho kililingana na sentimita 51.8 (inchi 20.4). Angalia Nyongeza B14.
Au “mikono 20 kufikia upana wa nyumba.”
Kipimo kisichojulikana.
Tnn., “nyumba.”
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “nyumba.”
Yaani, zikielekea Patakatifu.
Au “kusini.”
Au “kaskazini.”
Maana yake “Naye [yaani, Yehova] Aimarishe Kabisa.”
Labda inamaanisha “Katika Nguvu.”
Au “tangi.”
Karibu sentimita 7.4 (inchi 2.9). Angalia Nyongeza B14.
Bathi ilikuwa sawa na lita 22. Angalia Nyongeza B14.
Au “mikokoteni kumi ya maji.”
Wingi wa kifaa kinachoitwa uma.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, Sherehe ya Vibanda.
Au “makuhani Walawi.”
Tnn., “mwana wako, atakayetoka katika viuno vyako.”
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Au “aliyetendewa dhambi akimweka chini ya laana.” Yaani, kiapo kinacholeta laana ikiwa mtu anaapa kwa uwongo au kukosa kutimiza kiapo hicho.
Tnn., “laana.”
Tnn., “laana.”
Tnn., “kuleta juu ya kichwa chake mwenyewe jambo alilotenda.”
Tnn., “kuwa mwadilifu.”
Au “umewatesa.”
Au “panzi.”
Tnn., “katika nchi ya malango yake.”
Au “sifa yako.”
Angalia Kamusi.
Au “inayohusu.”
Tnn., “usiugeuzie mbali uso wa.”
Huenda ni Walawi.
Au “njia ya kuingia Hamathi.”
Angalia Kamusi.
Siku ya kwanza baada ya sherehe hiyo, au siku ya 15.
Au “jumba la.”
Tnn., “hukumu.”
Tnn., “methali.”
Au “jumba lake.”
Tnn., “wana wa Israeli.”
Au “Vibanda vya Muda.”
Au “ilikuwa na mpangilio mzuri; ilikamilishwa.”
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Au “mafumbo.”
Tnn., “lililofichwa.”
Tnn., “hakubaki na roho yoyote ndani yake.”
Au “maneno.”
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Au “jumba la.”
Au labda, “pamoja na zawadi zilizolingana na thamani ya.”
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Kwa kawaida ilibebwa na wapiga mishale.
Katika Maandiko ya Kiebrania mina moja inalingana na gramu 570. Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “waliutafuta uso wa.”
Au “wapanda farasi.”
Au “inayokandamiza.”
Tnn., “mahema yao.”
Tnn., “waliochaguliwa.”
Au “akaimarisha.”
Tnn., “mbuzi.”
Tnn., “uelewaji.”
Au “kuwasambaza.”
Tnn., “kutumikia falme za.”
Au “jumba la.”
Tnn., “wakimbiaji.”
Tnn., “waliochaguliwa.”
Tnn., “waliochaguliwa.”
Yaani, agano linalodumu na lisilobadilika.
Tnn., “aliyeujaza mkono wake na.”
Yaani, mikate ya wonyesho.
Tnn., “waliochaguliwa.”
Tnn., “walimwegemea.”
Tnn., “nguvu.”
Au “ufafanuzi wa; maelezo ya.”
Tnn., “ilipumzika.”
Angalia Kamusi.
Tnn., “milango miwili-miwili.”
Kwa kawaida ilibebwa na wapiga mishale.
Tnn., “kukanyaga upinde.”
Tnn., “tunakuegemea.”
Tnn., “siku nyingi.”
Tnn., “hakukuwa na amani kwa yule aliyetoka nje au kuingia ndani.”
Tnn., “msilegeze mikono.”
Angalia Kamusi.
Yaani, kingono.
Angalia Kamusi.
Au “ulikuwa na ujitoaji kamili.”
Tnn., “siku zake zote.”
Au “kuimarisha; kujenga upya.”
Au “asiondoke wala kuingia katika eneo la.”
Au “jumba la.”
Au “agano.”
Au “agano lako.”
Au “kuimarisha; kujenga upya.”
Au “kuimarisha; kujenga upya.”
Tnn., “ulimwegemea.”
Tnn., “hukumwegemea.”
Au “utegemezo wake.”
Au “una ujitoaji kamili.”
Tnn., “katika nyumba ya mikatale.”
Au “marhamu.”
Inaonekana kwamba hawakuichoma maiti ya Asa, bali walichoma vikolezo vyenye manukato.
Tnn., “kutembea katika.”
Angalia Kamusi.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Au “akamshawishi.”
Au “utawasukuma.”
Au “malaika.”
Au “bila nia mbaya.”
Tnn., “kambini.”
Au “jumba lake la kifalme.”
Angalia Kamusi.
Au “na moyo wako umeazimia.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Au “moyo wenye ujitoaji kamili.”
Au “awe na kilicho chema.”
Au labda, “Wameuni.”
Inaonekana ni Bahari ya Chumvi.
Tnn., “akauelekeza uso wake.”
Tnn., “mbegu ya.”
Au “korongo.”
Au “muone jinsi Yehova atakavyowaokoa.”
Au “kuvumilia.”
Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”
Tnn., “walimbariki.”
Maana yake “Baraka.”
Tnn., “Hujatembea katika.”
Tnn., “akaichochea roho ya.”
Au “jumba la.”
Anaitwa pia Ahazia.
Tnn., “binti ya.”
Anaitwa “Azaria,” katika baadhi ya hati za Kiebrania.
Au “alikuwa mgonjwa.”
Tnn., “mwana.”
Tnn., “mbegu yote ya ufalme.”
Au “agano.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Au “jumba la.”
Tnn., “anapotoka nje na anapoingia ndani.”
Kwa kawaida ilibebwa na wapiga mishale.
Labda ni kitabu cha kukunjwa kilichokuwa na Sheria ya Mungu.
Au “walitoa ishara ya kutoa sifa.”
Au “jumba la.”
Au “hekalu la Baali na kulibomoa.”
Tnn., “kwa mikono ya.”
Au “jumba la.”
Au labda, “wote walipokuwa wametoa.”
Angalia Kamusi.
Tnn., “kulikuwa na hasira.”
Au “kutoa ushahidi dhidi yao.”
Au “ikamfunika.”
Yaani, baba ya Zekaria.
Yaani, Wasiria.
Au “akiwa na magonjwa mengi.”
Au “mwana.” Huenda wingi unaonyesha utukufu.
Tnn., “kuweka msingi wa.”
Au “ufafanuzi wa; maelezo ya.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Tnn., “waliochaguliwa.”
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Au “tukutane uso kwa uso.”
Au “jumba lako mwenyewe la kifalme.”
Tnn., “katika hema lake.”
Anaitwa pia Ahazia.
Karibu mita 178 (futi 584). Angalia Nyongeza B14.
Au “jumba la.”
Yaani, Amazia baba yake.
Inaelekea alichimba kwenye miamba.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Au “jumba la.”
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Kori moja ilikuwa sawa na lita 220 (kilogramu 170 hivi). Angalia Nyongeza B14.
Au “alizitayarisha.”
Au “sanamu za kuyeyushwa.”
Angalia Kamusi, “Gehena.”
Tnn., “nyumba.”
Au “jumba la.”
Au “kudhihakiwa.”
Au “kupumzika.”
Yaani, mikate ya wonyesho.
Tnn., “Sasa mmeujaza mkono wenu.”
Tnn., “walikuwa na moyo mnyoofu katika.”
Au “ukatayarishwa.”
Au “ghafla.”
Tnn., “wakimbiaji.”
Au “neema.”
Tnn., “wakimbiaji.”
Tnn., “kuwapa moyo mmoja.”
Tnn., “akawaponya.”
Tnn., “akazungumza na moyo wao.”
Angalia Kamusi.
Tnn., “kambi.”
Au “wajitoe kikamili kwa.”
Au “vyumba vya kulia chakula.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Au “Milo.” Neno la Kiebrania linalomaanisha “jaza.”
Tnn., “akazungumza na moyo wao.”
Au “nguvu za mwanadamu.”
Au “uwezo wake wote wa kijeshi na fahari.”
Au “hekalu la.”
Au “kumfanyia muujiza.”
Au “muujiza uliokuwa umetokea.”
Angalia Kamusi.
Tnn., “aliwapitisha.”
Au “alibashiri.”
Tnn., “maamuzi ya hukumu niliyowapa.”
Au labda, “mashimoni.”
Au “aliutuliza uso wa Yehova Mungu wake.”
Au “kwenye korongo.”
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Au “sanamu za kuyeyushwa.”
Angalia Kamusi.
Au “sanamu za kuyeyushwa.”
Angalia Kamusi.
Tnn., “nyumba.”
Au “waliobeba mizigo.”
Tnn., “kwa mkono wa.”
Tnn., “Wamemimina.”
Tnn., “laini.”
Tnn., “nitakukusanya kwa mababu zako.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.
Au “kufanya upya lile agano.”
Angalia Kamusi.
Au “akaondoa miungu yote.”
Tnn., “Siku zake zote.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Tnn., “wana wa watu.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Au labda, “Waliichoma.”
Tnn., “nyumba.”
Au “maombolezo.”
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Labda, majira ya kuchipua.
Tnn., “akafanya shingo yake iwe ngumu.”