Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt 1 Wafalme 1:1-22:53
  • 1 Wafalme

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • 1 Wafalme
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
1 Wafalme

KITABU CHA KWANZA CHA WAFALME

1 Sasa Mfalme Daudi alikuwa amezeeka,+ umri wake ulikuwa umesonga,* na ingawa walimfunika kwa nguo, hakuweza kupata joto. 2 Kwa hiyo watumishi wake wakamwambia: “Bwana wetu mfalme turuhusu tukutafutie msichana bikira atakayekuhudumia na kukutunza. Atalala mikononi mwako ili bwana wetu mfalme upate joto.” 3 Wakatafuta msichana mrembo katika eneo lote la Israeli, wakampata Abishagi,+ Mshunamu,+ wakamleta kwa mfalme. 4 Msichana huyo alikuwa mrembo sana, naye alimhudumia mfalme na kumtunza, lakini mfalme hakufanya naye ngono.

5 Wakati huo, Adoniya+ mwana wa Hagithi alikuwa akijikweza, akisema: “Nitakuwa mfalme!” Alijitengenezea gari, naye akawa na wapanda farasi na wanaume 50 waliokimbia mbele yake.+ 6 Lakini baba yake hakuwahi kamwe kumkemea* kwa kumuuliza: “Kwa nini umefanya hivi?” Alikuwa pia na sura nzuri sana, na mama yake alimzaa baada ya Absalomu. 7 Alishauriana na Yoabu mwana wa Seruya na kuhani Abiathari,+ nao wakajitolea kumsaidia Adoniya na kumuunga mkono.+ 8 Lakini kuhani Sadoki,+ Benaya+ mwana wa Yehoyada, nabii Nathani,+ Shimei,+ Rei, na wale mashujaa hodari wa Daudi+ hawakumuunga mkono Adoniya.

9 Mwishowe Adoniya akawatoa dhabihu+ kondoo, ng’ombe, na wanyama waliononeshwa, kando ya jiwe la Zohelethi, lililo karibu na En-rogeli, akawaalika ndugu zake wote wana wa mfalme, na wanaume wote wa Yuda watumishi wa mfalme. 10 Lakini hakumwalika nabii Nathani, Benaya na wale mashujaa hodari, wala Sulemani ndugu yake. 11 Ndipo Nathani+ akamuuliza Bath-sheba,+ mama ya Sulemani:+ “Je, hujasikia kwamba Adoniya+ mwana wa Hagithi amekuwa mfalme, na bwana wetu Daudi hajui lolote kuhusu jambo hilo? 12 Sasa, njoo tafadhali, nikupe ushauri, ili uokoe uhai wako mwenyewe na uhai wa* mwana wako Sulemani.+ 13 Nenda kwa Mfalme Daudi ukamuulize, ‘Je, bwana wangu mfalme, hukuniapia mimi kijakazi wako, ukisema: “Sulemani mwana wako atakuwa mfalme baada yangu, naye ndiye atakayeketi kwenye kiti changu cha ufalme”?+ Basi kwa nini Adoniya amekuwa mfalme?’ 14 Utakapokuwa ukiendelea kuzungumza na mfalme, nitaingia na kuthibitisha maneno yako.”

15 Kwa hiyo Bath-sheba akaingia kwa mfalme, katika chumba chake cha faragha. Mfalme alikuwa amezeeka sana, na Abishagi,+ Mshunamu, alikuwa akimhudumia mfalme. 16 Kisha Bath-sheba akainama na kumsujudia mfalme, mfalme akamuuliza: “Una ombi gani?” 17 Akajibu: “Bwana wangu, wewe ndiye uliyeniapia mimi kijakazi wako kwa jina la Yehova Mungu wako uliposema, ‘Sulemani mwana wako atakuwa mfalme baada yangu, na ndiye atakayeketi kwenye kiti changu cha ufalme.’+ 18 Lakini tazama! Adoniya amekuwa mfalme, na bwana wangu mfalme hujui lolote kuhusu jambo hilo.+ 19 Aliwatoa dhabihu ng’ombe dume, wanyama waliononeshwa, na kondoo wengi sana na kuwaalika wana wote wa mfalme na kuhani Abiathari na Yoabu mkuu wa jeshi;+ lakini hakumwalika Sulemani mtumishi wako.+ 20 Na sasa, bwana wangu mfalme, macho yote ya Waisraeli yanakutazama uwaambie ni nani atakayeketi kwenye kiti chako cha ufalme baada yako bwana wangu mfalme. 21 Usipofanya hivyo, mara tu utakapokufa na kuzikwa pamoja na mababu zako bwana wangu mfalme, mimi na mwanangu Sulemani tutaonwa kuwa wasaliti.”

22 Na alipokuwa akiendelea kuzungumza na mfalme, nabii Nathani akaingia.+ 23 Mara moja mfalme akaambiwa hivi: “Nabii Nathani amefika!” Akaingia mbele ya mfalme na kumsujudia mfalme mpaka ardhini. 24 Kisha Nathani akasema: “Bwana wangu mfalme, je, ulisema hivi: ‘Adoniya atakuwa mfalme baada yangu, na ndiye atakayeketi kwenye kiti changu cha ufalme’?+ 25 Kwa maana leo ameshuka kwenda kuwatoa dhabihu+ ng’ombe dume, wanyama waliononeshwa, na kondoo wengi sana, naye amewaalika wana wote wa mfalme na wakuu wa jeshi na kuhani Abiathari.+ Wako huko wakila na kunywa pamoja naye, nao wanaendelea kusema, ‘Mfalme Adoniya na aishi muda mrefu!’ 26 Lakini hakunialika mimi mtumishi wako, wala kuhani Sadoki, wala Benaya+ mwana wa Yehoyada, wala Sulemani mtumishi wako. 27 Je, bwana wangu mfalme umeidhinisha jambo hili bila kuniambia mimi mtumishi wako ni nani anayepaswa kuketi kwenye kiti chako cha ufalme baada yako?”

28 Ndipo Mfalme Daudi akajibu: “Niitieni Bath-sheba.” Basi akaingia na kusimama mbele ya mfalme. 29 Kisha mfalme akaapa hivi: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, aliyeniokoa* kutoka katika mateso yangu yote,+ 30 kama nilivyokuapia kwa jina la Yehova Mungu wa Israeli, nikisema, ‘Sulemani mwana wako atakuwa mfalme baada yangu, na ndiye atakayeketi kwenye kiti changu cha ufalme baada yangu!’ hivyo ndivyo nitakavyofanya siku ya leo.” 31 Ndipo Bath-sheba akainama mpaka ardhini na kumsujudia mfalme na kusema: “Bwana wangu Mfalme Daudi na aishi milele!”

32 Mara moja Mfalme Daudi akasema: “Niitieni kuhani Sadoki, nabii Nathani, na Benaya+ mwana wa Yehoyada.”+ Basi wakaja mbele ya mfalme. 33 Mfalme akawaambia: “Nendeni na watumishi wangu, mkampandishe Sulemani mwanangu juu ya nyumbu* wangu mwenyewe,+ mteremsheni hadi Gihoni.+ 34 Kuhani Sadoki na nabii Nathani watamtia mafuta+ huko awe mfalme wa Israeli; kisha pigeni pembe na kusema, ‘Mfalme Sulemani na aishi muda mrefu!’+ 35 Kisha mfuateni anaporudi, naye atakuja na kuketi kwenye kiti changu cha ufalme; atakuwa mfalme baada yangu, nami nitamweka rasmi kuwa kiongozi wa Israeli na wa Yuda.” 36 Mara moja Benaya mwana wa Yehoyada akamwambia mfalme: “Amina! Yehova Mungu wako bwana wangu mfalme na athibitishe jambo hilo. 37 Kama Yehova alivyokuwa pamoja nawe bwana wangu mfalme, na awe pia na Sulemani,+ na Afanye kiti chake cha ufalme kiwe kikuu zaidi kuliko kiti chako cha ufalme, bwana wangu Mfalme Daudi.”+

38 Kisha kuhani Sadoki, nabii Nathani, Benaya+ mwana wa Yehoyada, na Wakerethi na Wapelethi+ wakateremka, nao wakampandisha Sulemani juu ya nyumbu wa Mfalme Daudi,+ wakampeleka Gihoni.+ 39 Kisha Kuhani Sadoki akachukua pembe ya mafuta+ kutoka hemani+ na kumtia mafuta Sulemani,+ nao wakaanza kupiga pembe, na watu wote wakaanza kusema hivi kwa sauti kubwa: “Mfalme Sulemani na aishi muda mrefu!” 40 Kisha watu wote wakapanda wakimfuata, wakipiga filimbi na kushangilia sana, hivi kwamba dunia ikapasuka na kufunguka kwa sababu ya kelele zao.+

41 Adoniya na watu wote aliowaalika wakasikia kelele hizo walipokuwa wamemaliza kula.+ Mara tu Yoabu aliposikia sauti ya pembe, akauliza: “Kwa nini kuna kelele za vurugu jijini?” 42 Alipokuwa bado anaongea, Yonathani+ mwana wa kuhani Abiathari akaja. Kisha Adoniya akamwambia: “Ingia, kwa maana wewe ni mtu mwema,* bila shaka unaleta habari njema.” 43 Lakini Yonathani akamjibu Adoniya: “Hapana! Bwana wetu Mfalme Daudi amemweka Sulemani kuwa mfalme. 44 Mfalme alimwagiza aende pamoja na kuhani Sadoki, nabii Nathani, Benaya mwana wa Yehoyada, na Wakerethi na Wapelethi, nao wakampandisha juu ya nyumbu wa mfalme.+ 45 Kisha kuhani Sadoki na nabii Nathani wakamtia mafuta kuwa mfalme huko Gihoni. Halafu wakapanda kutoka huko wakishangilia, nalo jiji limejaa kelele. Hizo ndizo kelele mlizosikia. 46 Isitoshe, Sulemani ameketi kwenye kiti cha ufalme. 47 Na tena, watumishi wa mfalme wamekuja kumpongeza bwana wetu Mfalme Daudi, wakisema, ‘Mungu wako na alifanye jina la Sulemani liwe na fahari kuliko jina lako, na Akifanye kiti chake cha ufalme kiwe kikuu kuliko kiti chako cha ufalme!’ Ndipo mfalme akainama kitandani. 48 Na pia mfalme akasema, ‘Yehova Mungu wa Israeli na asifiwe, ambaye leo amemchagua mtu wa kuketi kwenye kiti changu cha ufalme na ameruhusu macho yangu mwenyewe yaone jambo hilo!’”

49 Basi watu wote walioalikwa na Adoniya wakaogopa sana, na kila mmoja wao akainuka na kwenda zake. 50 Adoniya aliogopa pia kwa sababu ya Sulemani, basi akaondoka, akaenda na kuzishika kwa nguvu pembe za madhabahu.+ 51 Sulemani akaletewa habari hii: “Tazama! Adoniya anamwogopa Mfalme Sulemani; naye ameshika pembe za madhabahu, akisema, ‘Mfalme Sulemani na aniapie kwanza kwamba hataniua mimi mtumishi wake kwa upanga.’” 52 Ndipo Sulemani akasema: “Akitenda kwa njia inayofaa, hakuna unywele wake hata mmoja utakaoanguka ardhini; lakini akipatikana ametenda uovu,+ lazima afe.” 53 Basi Mfalme Sulemani akaagiza aletwe kutoka kwenye madhabahu. Ndipo akaingia na kumwinamia Mfalme Sulemani, kisha Sulemani akamwambia: “Nenda nyumbani kwako.”

2 Daudi alipokaribia kufa, alimpa Sulemani mwanawe maagizo haya: 2 “Nakaribia kufa.* Kwa hiyo, uwe imara+ na ujithibitishe kuwa mwanamume.+ 3 Ni lazima utimize wajibu wako kwa Yehova Mungu wako kwa kutembea katika njia zake na kushika maagizo yake, amri zake, sheria zake,* na vikumbusho vyake kama vilivyoandikwa katika Sheria ya Musa;+ ndipo utakapofanikiwa* katika kila jambo unalofanya na kila mahali unapogeuka kwenda. 4 Na Yehova atatimiza ahadi aliyotoa kunihusu aliposema hivi: ‘Ikiwa wana wako wataikazia uangalifu njia yao kwa kutembea kwa uaminifu mbele zangu kwa moyo wao wote na kwa nafsi* yao yote,+ hutakosa kamwe mwanamume wa uzao wako atakayeketi kwenye kiti cha ufalme cha Israeli.’+

5 “Pia unajua vizuri jambo ambalo Yoabu mwana wa Seruya alinitendea, jambo alilowatendea wakuu wawili wa majeshi ya Israeli, Abneri+ mwana wa Neri na Amasa+ mwana wa Yetheri. Aliwaua, na hivyo akamwaga damu+ ya vita wakati wa amani, akapaka damu ya vita kwenye mshipi uliokuwa kiunoni mwake na kwenye viatu alivyokuwa amevaa miguuni. 6 Ni lazima utende kulingana na hekima yako, nawe usimruhusu ashuke Kaburini* kwa amani akiwa amezeeka.*+

7 “Lakini watendee wana wa Barzilai+ Mgileadi kwa upendo mshikamanifu, nao wanapaswa kuwa miongoni mwa wale wanaokula mezani pako, kwa maana hivyo ndivyo walivyonisaidia+ nilipomkimbia Absalomu ndugu yako.+

8 “Pia, Shimei mwana wa Gera, Mbenjamini, kutoka Bahurimu yuko pamoja nawe. Yeye ndiye aliyenitukana vikali+ siku niliyokuwa nikienda Mahanaimu;+ lakini aliposhuka kuja kunipokea kwenye Mto Yordani, nilimwapia hivi kwa jina la Yehova: ‘Sitakuua kwa upanga.’+ 9 Sasa usikose kumwadhibu,+ kwa maana wewe ni mtu mwenye hekima nawe unajua unalopaswa kumtendea; usimruhusu azeeke na kushuka Kaburini.”**+

10 Kisha Daudi akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi.+ 11 Daudi alitawala Israeli kwa miaka 40. Alitawala Hebroni+ kwa miaka 7, na Yerusalemu kwa miaka 33.+

12 Kisha Sulemani akaketi kwenye kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, na ufalme wake ukaimarishwa kabisa hatua kwa hatua.+

13 Baada ya muda Adoniya mwana wa Hagithi akaja kwa Bath-sheba, mama ya Sulemani. Bath-sheba akamuuliza: “Je, umekuja kwa amani?” Akamjibu: “Ni kwa amani.” 14 Adoniya akasema: “Ningependa kukwambia jambo fulani.” Basi akamwambia: “Sema.” 15 Adoniya akasema: “Unajua vizuri kwamba ufalme ulipaswa kuwa wangu, na Waisraeli wote walitarajia niwe mfalme;+ lakini ufalme uliniponyoka ukawa wa ndugu yangu, kwa maana Yehova ndiye aliyempa.+ 16 Lakini sasa nakuomba jambo moja tu. Usikatae ombi langu.” Basi Bath-sheba akamwambia: “Sema.” 17 Adoniya akasema: “Tafadhali, mwombe Mfalme Sulemani—kwa maana hawezi kukataa ombi lako—anipe Abishagi,+ Mshunamu, awe mke wangu.” 18 Ndipo Bath-sheba akasema: “Sawa kabisa! Nitazungumza na mfalme kwa niaba yako.”

19 Kwa hiyo Bath-sheba akaenda kuzungumza na Mfalme Sulemani kwa niaba ya Adoniya. Mara moja mfalme akainuka ili kumpokea, akamwinamia. Kisha akaketi kwenye kiti chake cha ufalme, akaagiza pia mama yake aletewe kiti cha ufalme, ili aketi upande wake wa kulia. 20 Bath-sheba akasema: “Nina ombi moja dogo. Usikatae ombi langu.” Basi mfalme akamwambia: “Mama yangu, sema ombi lako; kwa sababu sitalikataa.” 21 Akasema: “Mruhusu Abishagi, Mshunamu, awe mke wa Adoniya ndugu yako.” 22 Ndipo Mfalme Sulemani akamjibu mama yake: “Kwa nini unaomba Abishagi Mshunamu awe mke wa Adoniya? Huenda ukamwombea pia ufalme,+ kwa sababu yeye ni ndugu yangu mkubwa,+ naye anaungwa mkono na kuhani Abiathari na Yoabu+ mwana wa Seruya.”+

23 Kwa hiyo Mfalme Sulemani akaapa hivi kwa jina la Yehova: “Mungu na aniadhibu, tena vikali, ikiwa Adoniya hakuomba jambo hilo akijua kwamba anahatarisha uhai wake.* 24 Na sasa, kwa hakika kama Yehova anavyoishi, ambaye ameniimarisha kabisa+ na kuniketisha kwenye kiti cha ufalme cha Daudi baba yangu na kunijengea nyumba* kama alivyoahidi,+ Adoniya atauawa+ leo.” 25 Mara moja Mfalme Sulemani akamtuma Benaya+ mwana wa Yehoyada, akatoka na kwenda kumpiga Adoniya, akafa.

26 Mfalme akamwambia kuhani Abiathari:+ “Nenda Anathothi+ kwenye mashamba yako! Unastahili kufa, lakini leo sitakuua kwa sababu ulibeba Sanduku la Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mbele ya baba yangu Daudi+ na kwa sababu ulishiriki katika mateso yote ya baba yangu.”+ 27 Basi Sulemani akamwondoa Abiathari asiendelee kutumikia akiwa kuhani wa Yehova, ili kutimiza neno ambalo Yehova alisema dhidi ya nyumba ya Eli+ kule Shilo.+

28 Habari hizo zilipomfikia Yoabu—kwa maana Yoabu alikuwa amemuunga mkono Adoniya+ lakini hakuwa amemuunga mkono Absalomu+—Yoabu akakimbilia katika hema la Yehova+ na kushika kwa nguvu pembe za madhabahu. 29 Kisha Mfalme Sulemani akaambiwa hivi: “Yoabu amekimbilia katika hema la Yehova, na yuko humo kando ya madhabahu.” Kwa hiyo Sulemani akamtuma Benaya mwana wa Yehoyada, akisema: “Nenda ukamuue!” 30 Basi Benaya akaenda katika hema la Yehova na kumwambia, “Mfalme anasema hivi: ‘Toka nje!’” Lakini Yoabu akasema: “Hapana! Nitafia hapa.” Benaya akarudi kwa mfalme na kumwambia: “Hivi ndivyo alivyosema Yoabu, na hivi ndivyo alivyonijibu.” 31 Kisha mfalme akamwambia: “Fanya kama alivyosema; muue na umzike, uniondolee mimi na nyumba ya baba yangu damu ambayo Yoabu alimwaga kwa njia isiyo ya haki.+ 32 Yehova atamlipiza kwa sababu ya damu aliyomwaga,* kwa sababu bila Daudi baba yangu kujua, aliwapiga na kuwaua kwa upanga wanaume wawili walio waadilifu na bora kuliko yeye, yaani, Abneri+ mwana wa Neri mkuu wa jeshi la Israeli,+ na Amasa+ mwana wa Yetheri, mkuu wa jeshi la Yuda.+ 33 Hatia ya damu yao itakuwa juu ya kichwa cha Yoabu na juu ya kichwa cha uzao* wake milele;+ lakini amani kutoka kwa Yehova na iwe milele juu ya Daudi, uzao* wake, nyumba yake, na kiti chake cha ufalme.” 34 Kisha Benaya mwana wa Yehoyada akapanda kwenda huko, akampiga Yoabu na kumuua, akazikwa nyumbani kwake nyikani. 35 Halafu mfalme akamweka Benaya+ mwana wa Yehoyada kuwa mkuu wa jeshi baada yake, na mfalme akamweka Sadoki+ kuwa kuhani badala ya Abiathari.

36 Kisha mfalme akamwita Shimei+ na kumwambia: “Jijengee nyumba Yerusalemu, uishi huko; usitoke huko na kwenda mahali pengine popote. 37 Siku utakapotoka na kuvuka Bonde la Kidroni,+ ujue kwa hakika kwamba utakufa. Damu yako itakuwa juu ya kichwa chako mwenyewe.” 38 Shimei akamwambia mfalme: “Jambo ulilosema si baya. Mimi mtumishi wako nitafanya kama ulivyosema bwana wangu mfalme.” Basi Shimei akakaa Yerusalemu kwa siku nyingi.

39 Lakini baada ya miaka mitatu, watumwa wawili wa Shimei wakatoroka na kwenda kwa Akishi+ mwana wa Maaka mfalme wa Gathi. Shimei alipoambiwa, “Tazama! Watumwa wako wameenda Gathi,” 40 mara moja Shimei akaweka matandiko juu ya punda wake, akaenda Gathi kwa Akishi kuwatafuta watumwa wake. Shimei aliporudi kutoka Gathi pamoja na watumwa wake, 41 Sulemani akaambiwa: “Shimei aliondoka Yerusalemu na kwenda Gathi, naye amerudi.” 42 Ndipo mfalme akamwita Shimei na kumuuliza: “Je, sikukuapisha kwa jina la Yehova na kukuonya kwa kusema, ‘Siku utakapotoka hapa na kwenda mahali pengine popote, ujue kwa hakika kwamba utakufa’? Na je, wewe hukuniambia, ‘Jambo ulilosema ni sawa; nitatii’?+ 43 Kwa nini basi, hukutii kiapo cha Yehova na amri niliyokupa?” 44 Kisha mfalme akamwambia Shimei: “Unajua moyoni mwako madhara yote uliyomtendea baba yangu Daudi,+ basi Yehova atakulipiza kwa sababu ya madhara hayo.*+ 45 Lakini mimi Mfalme Sulemani nitabarikiwa,+ na kiti cha ufalme cha Daudi kitaimarishwa kabisa mbele za Yehova milele.” 46 Ndipo mfalme akamwamuru Benaya mwana wa Yehoyada, basi akatoka nje na kumpiga Shimei, akamuua.+

Hivyo, ufalme ukaimarishwa kabisa mikononi mwa Sulemani.+

3 Sulemani alifanya mapatano ya ndoa na Farao mfalme wa Misri. Alimwoa* binti ya Farao+ na kumleta katika Jiji la Daudi+ mpaka alipomaliza kujenga nyumba yake mwenyewe,+ na nyumba ya Yehova,+ na ukuta kuzunguka Yerusalemu.+ 2 Lakini bado watu walikuwa wakitoa dhabihu mahali pa juu,+ kwa maana kufikia wakati huo nyumba haikuwa imejengwa kwa ajili ya jina la Yehova.+ 3 Sulemani akaendelea kumpenda Yehova kwa kutembea katika sheria za Daudi baba yake, ila tu alikuwa akitoa dhabihu na kufanya matoleo yafuke moshi mahali pa juu.+

4 Mfalme alienda Gibeoni kutoa dhabihu huko, kwa maana ndipo palipokuwa mahali maarufu* zaidi pa juu.+ Sulemani alitoa dhabihu 1,000 za kuteketezwa juu ya madhabahu hiyo.+ 5 Huko Gibeoni, Yehova alimtokea Sulemani katika ndoto usiku na kumwambia: “Niombe unachotaka nikupe.”+ 6 Basi Sulemani akasema: “Umemtendea mtumishi wako Daudi baba yangu kwa upendo mwingi mshikamanifu alipokuwa akitembea mbele zako kwa uaminifu na kwa uadilifu na kwa unyoofu wa moyo. Umeendelea kumtendea kwa upendo huo mwingi mshikamanifu mpaka leo hii kwa kumpa mwana aketi kwenye kiti chake cha ufalme.+ 7 Na sasa, Yehova Mungu wangu, umeniweka mimi mtumishi wako niwe mfalme baada ya Daudi baba yangu, ingawa mimi ni kijana* tu na sina uzoefu.*+ 8 Mimi mtumishi wako ni miongoni mwa watu wako uliowachagua,+ watu wengi sana hivi kwamba hawawezi kuhesabiwa wala idadi yao kujulikana. 9 Basi nipe mimi mtumishi wako moyo mtiifu ili niwahukumu watu wako,+ nitofautishe mema na mabaya,+ kwa sababu ni nani anayeweza kuwahukumu watu hawa wako ambao ni wengi sana?”*

10 Ombi hilo la Sulemani lilimpendeza Yehova.+ 11 Basi Mungu akamwambia: “Kwa kuwa umeomba jambo hili, nawe hukujiombea maisha marefu* wala utajiri wala kuomba maadui wako wafe, lakini uliomba uelewaji wa kusikiliza kesi,+ 12 nitafanya uliloomba.+ Nitakupa moyo wenye hekima na uelewaji,+ hivi kwamba kama vile ambavyo hajawahi kamwe kuwapo mtu mwingine kama wewe kabla yako, hatawahi kamwe kuwapo mtu mwingine kama wewe baada yako.+ 13 Isitoshe, nitakupa vitu ambavyo hukuomba,+ utajiri na utukufu,+ hivi kwamba hatakuwapo mfalme mwingine kama wewe katika maisha yako yote.*+ 14 Nawe ukitembea katika njia zangu kwa kushika masharti yangu na amri zangu, kama Daudi baba yako alivyotembea,+ nitakupa pia maisha marefu.”*+

15 Sulemani alipoamka, aligundua kwamba ilikuwa ndoto. Kisha akaenda Yerusalemu, akasimama mbele ya sanduku la agano la Yehova, akatoa dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ushirika+ na kuwaandalia karamu watumishi wake wote.

16 Wakati huo makahaba wawili wakaja kwa mfalme na kusimama mbele yake. 17 Mwanamke wa kwanza akasema: “Tafadhali, bwana wangu, mimi na mwanamke huyu tunaishi katika nyumba moja, nami nilizaa mtoto alipokuwa nyumbani. 18 Siku ya tatu baada ya mimi kuzaa mtoto, mwanamke huyu pia alizaa mtoto. Tulikuwa pamoja, sisi wawili tu; hapakuwa na mtu mwingine yeyote nyumbani. 19 Usiku, mwana wa mwanamke huyu akafa, kwa sababu alimlalia. 20 Basi akaamka katikati ya usiku, akamchukua mwanangu kutoka kando yangu mimi kijakazi wako nilipokuwa nimelala usingizi, akamlaza mikononi mwake,* kisha akamlaza mwana wake mfu mikononi mwangu. 21 Nilipoamka asubuhi ili kumnyonyesha mwanangu, nikaona amekufa. Kwa hiyo nikamchunguza kwa makini, nikagundua kwamba hakuwa mwanangu niliyemzaa.” 22 Lakini mwanamke huyo mwingine akasema: “Hapana, aliye hai ni mwanangu na aliyekufa ndiye mwanao!” Lakini mwanamke wa kwanza aliendelea kusema: “Hapana, aliyekufa ndiye mwanao, na mwanangu ndiye aliye hai.” Hivyo ndivyo walivyobishana mbele ya mfalme.

23 Mwishowe mfalme akasema: “Huyu anasema, ‘Huyu aliye hai ni mwanangu, aliyekufa ni mwanao!’ na huyu anasema, ‘Hapana, aliyekufa ni mwanao, aliye hai ni mwanangu!’” 24 Mfalme akasema: “Nileteeni upanga.” Basi wakamletea mfalme upanga. 25 Kisha mfalme akasema: “Mkateni vipande viwili mtoto aliye hai, mpeni mwanamke mmoja nusu moja na nusu nyingine mpeni mwingine.” 26 Mara moja mwanamke ambaye ni mama ya mtoto aliye hai akamsihi mfalme, kwa maana alishikwa na huruma kwa ajili ya mwanawe. Akasema: “Tafadhali, bwana wangu! Mpe yeye mtoto aliye hai! Usimuue kamwe.” Lakini yule mwanamke mwingine alikuwa akisema: “Hatakuwa wako wala hatakuwa wangu. Acha wamkate vipande viwili!” 27 Ndipo mfalme akasema: “Mpeni mwanamke wa kwanza mtoto aliye hai! Msimuue kamwe, kwa maana yeye ndiye mama yake.”

28 Kwa hiyo Waisraeli wote wakasikia kuhusu uamuzi uliofanywa na mfalme, nao wakamwogopa mfalme,+ kwa maana waliona kwamba alikuwa na hekima ya Mungu katika kutekeleza haki.+

4 Mfalme Sulemani alitawala Israeli yote.+ 2 Hawa ndio waliokuwa maofisa wake wakuu:* Azaria mwana wa Sadoki+ alikuwa kuhani; 3 Elihorefu na Ahiya wana wa Shisha walikuwa waandishi;+ Yehoshafati+ mwana wa Ahiludi alifanya kazi ya kuweka kumbukumbu; 4 Benaya+ mwana wa Yehoyada alikuwa mkuu wa jeshi; Sadoki na Abiathari+ walikuwa makuhani; 5 Azaria mwana wa Nathani+ alikuwa mkuu wa wasaidizi; Zabudi mwana wa Nathani alikuwa kuhani na rafiki ya mfalme;+ 6 Ahishari alikuwa msimamizi wa nyumba; na Adoniramu+ mwana wa Abda aliwasimamia wale walioandikishwa kufanya kazi ya kulazimishwa.+

7 Sulemani alikuwa na wasaidizi 12 waliowasimamia Waisraeli wote waliomwandalia chakula mfalme na nyumba yake. Kila mmoja wao alikuwa na jukumu la kuandaa chakula mwezi mmoja kwa mwaka.+ 8 Haya ndiyo majina yao: Mwana wa Huru, katika eneo lenye milima la Efraimu; 9 mwana wa Dekeri, kule Makazi, Shaalbimu,+ Beth-shemeshi, na Elon-beth-hanani; 10 mwana wa Hesedi, kule Arubothi (alisimamia Soko na nchi yote ya Heferi); 11 mwana wa Abinadabu, katika milima yote ya Dori (Tafathi, binti ya Sulemani, akawa mke wake); 12 Baana mwana wa Ahiludi, kule Taanaki, Megido,+ na eneo lote la Beth-sheani,+ ambalo liko kando ya Sarethani chini ya Yezreeli, kuanzia Beth-sheani mpaka Abel-mehola hadi eneo la Yokmeamu;+ 13 mwana wa Geberi, kule Ramothi-gileadi+ (alisimamia vijiji vya mahema vya Yairi+ mwana wa Manase, vilivyoko Gileadi;+ alisimamia pia eneo la Argobu,+ lililoko Bashani:+ majiji makubwa 60 yenye kuta na makomeo ya shaba); 14 Ahinadabu mwana wa Ido, kule Mahanaimu;+ 15 Ahimaazi, kule Naftali (alimwoa Basemathi, binti mwingine wa Sulemani); 16 Baana mwana wa Hushai, kule Asheri na Bealothi; 17 Yehoshafati mwana wa Parua, kule Isakari; 18 Shimei+ mwana wa Ela, kule Benjamini;+ 19 Geberi mwana wa Uri, katika nchi ya Gileadi,+ nchi ya Sihoni+ mfalme wa Waamori, na ya Ogu+ mfalme wa Bashani. Kulikuwa pia na msaidizi mmoja aliyewasimamia wasaidizi hao wengine wote nchini.

20 Watu wa Yuda na Israeli walikuwa wengi sana kama chembe za mchanga kando ya bahari;+ walikuwa wakila na kunywa na kushangilia.+

21 Sulemani alitawala falme zote kuanzia Mto Efrati+ mpaka nchi ya Wafilisti hadi kwenye mpaka wa Misri. Walimletea Sulemani ushuru na kumtumikia siku zote za maisha yake.+

22 Chakula cha kila siku cha Sulemani kilikuwa kori 30* za unga laini na kori 60 za unga, 23 ng’ombe 10 waliononeshwa, ng’ombe 20 waliopelekwa malishoni, na kondoo 100, pamoja na paa kadhaa, swala, kulungu, na ndege waliononeshwa. 24 Kwa maana alitawala kila kitu upande huu wa Mto Efrati,*+ kuanzia Tifsa mpaka Gaza,+ pamoja na wafalme wote upande huu wa Mto Efrati; naye alikuwa na amani katika maeneo yake yote.+ 25 Watu wa Yuda na Israeli waliishi kwa usalama, kila mtu chini ya mzabibu wake mwenyewe na chini ya mtini wake mwenyewe, kuanzia Dani mpaka Beer-sheba, siku zote za Sulemani.

26 Na Sulemani alikuwa na mabanda 4,000* ya farasi wa magari yake ya vita, na farasi* 12,000.+

27 Wasaidizi hao walimletea chakula Mfalme Sulemani na pia kila mtu aliyekula mezani pa Mfalme Sulemani. Kila mmoja wao alikuwa na jukumu la kuleta chakula mwezi aliopangiwa na kuhakikisha kwamba hakuna chochote kilichokosekana.+ 28 Walipeleka pia shayiri na majani mahali popote yalipohitajiwa kwa ajili ya farasi na kwa ajili ya farasi waliokokota magari, kila mmoja kulingana na kiasi alichogawiwa.

29 Naye Mungu akampa Sulemani hekima na utambuzi mwingi sana na moyo wenye uelewaji mwingi kama mchanga kwenye ufuo wa bahari.+ 30 Hekima ya Sulemani ilizidi hekima ya watu wote wa Mashariki na hekima yote ya Misri.+ 31 Alikuwa na hekima kuliko mwanadamu mwingine yeyote; alikuwa na hekima kuliko Ethani+ Mwezra na Hemani,+ Kalkoli,+ na Darda, wana wa Maholi; umaarufu wake ulienea katika mataifa yote yaliyomzunguka.+ 32 Alitunga* methali 3,000+ na nyimbo zake+ zilikuwa 1,005. 33 Alizungumza kuhusu miti, kuanzia mwerezi wa Lebanoni mpaka mhisopo+ unaomea ukutani; alizungumza kuhusu wanyama,+ ndege,*+ viumbe wanaotambaa,*+ na samaki. 34 Watu kutoka katika mataifa yote walikuja kuisikia hekima ya Sulemani, pamoja na wafalme kutoka kotekote duniani waliokuwa wamesikia kuhusu hekima yake.+

5 Mfalme Hiramu wa Tiro+ aliposikia kwamba Sulemani ametiwa mafuta kuwa mfalme baada ya baba yake, aliwatuma watumishi wake kwa Sulemani, kwa maana sikuzote Hiramu alikuwa rafiki ya Daudi.*+ 2 Naye Sulemani akamtumia Hiramu ujumbe huu:+ 3 “Unajua vizuri kwamba baba yangu Daudi hakuweza kujenga nyumba kwa ajili ya jina la Yehova Mungu wake kwa sababu ya watu waliopigana vita naye pande zote, mpaka Yehova alipowaweka maadui wake chini ya nyayo za miguu yake.+ 4 Lakini sasa Yehova Mungu wangu amenipumzisha pande zote.+ Hakuna yeyote anayenipinga na hakuna jambo lolote baya linalotendeka.+ 5 Kwa hiyo ninakusudia kujenga nyumba kwa ajili ya jina la Yehova Mungu wangu, kama Yehova alivyomwahidi baba yangu Daudi, akisema: ‘Mwana wako ambaye nitamweka kwenye kiti chako cha ufalme baada yako ndiye atakayejenga nyumba kwa ajili ya jina langu.’+ 6 Sasa waamuru watu wako wanikatie mierezi ya Lebanoni.+ Watumishi wangu watafanya kazi pamoja na watumishi wako, nami nitawalipa watumishi wako mishahara kulingana na kiwango utakachoweka, kwa maana unajua kwamba hakuna yeyote kati yetu anayejua kukata miti kama Wasidoni.”+

7 Hiramu aliposikia maneno ya Sulemani, akashangilia sana na kusema: “Yehova na asifiwe leo, kwa maana amempa Daudi mwana mwenye hekima atawale taifa hili kubwa!”*+ 8 Basi Hiramu akampelekea Sulemani ujumbe huu: “Nimepokea ujumbe ulionitumia. Nitatimiza mambo yote unayotaka ili upate mbao za mierezi na za miberoshi.+ 9 Watumishi wangu watateremsha magogo kutoka Lebanoni hadi baharini, nami nitayafunga magogo hayo mafungu-mafungu ili yaelee baharini mpaka mahali utakaponiambia. Nitaagiza yafunguliwe, kisha unaweza kuyabeba. Na wewe utanipa chakula nitakachoomba kwa ajili ya nyumba yangu.”+

10 Basi Hiramu akampa Sulemani mbao zote za mierezi na za miberoshi ambazo Sulemani alihitaji. 11 Naye Sulemani akampa Hiramu kori 20,000* za ngano kuwa chakula kwa ajili ya nyumba yake na kori 20 za mafuta bora sana ya zeituni.* Hivyo ndivyo vitu ambavyo Sulemani alimpa Hiramu mwaka baada ya mwaka.+ 12 Yehova akampa Sulemani hekima, kama Alivyokuwa amemwahidi.+ Na kulikuwa na amani kati ya Hiramu na Sulemani, nao wakafanya mkataba* kati yao.

13 Mfalme Sulemani aliwaandikisha wanaume kutoka katika Israeli yote ili wafanye kazi ya kulazimishwa; wanaume 30,000 waliandikishwa.+ 14 Alikuwa akiwapeleka wanaume 10,000 Lebanoni kila mwezi kwa zamu. Walikaa Lebanoni kwa mwezi mmoja na kukaa nyumbani kwa miezi miwili; na Adoniramu+ aliwasimamia wale walioandikishwa kufanya kazi ya kulazimishwa. 15 Sulemani alikuwa na vibarua* 70,000 na watu 80,000 waliokata mawe+ milimani,+ 16 na pia wakuu wasaidizi+ 3,300 waliowasimamia wafanyakazi. 17 Kwa agizo la mfalme, walichimbua mawe makubwa, mawe yenye thamani,+ ili yachongwe+ na kutumiwa kujenga msingi+ wa nyumba hiyo. 18 Kwa hiyo wajenzi wa Sulemani na wajenzi wa Hiramu na Wagebali+ walikata mawe, na kutayarisha mbao na mawe ya kujengea nyumba hiyo.

6 Katika mwaka wa 480 baada ya Waisraeli* kutoka katika nchi ya Misri,+ mwaka wa nne baada ya Sulemani kuwekwa kuwa mfalme wa Israeli, mwezi wa Zivu*+ (yaani, mwezi wa pili), Sulemani alianza kujenga nyumba ya Yehova.*+ 2 Nyumba ambayo Mfalme Sulemani alimjengea Yehova ilikuwa na urefu wa mikono 60,* upana wa mikono 20, na kimo cha mikono 30.+ 3 Ukumbi+ wa mbele wa hekalu* ulikuwa na urefu* wa mikono 20, nao ulilingana na upana wa nyumba. Ulikuwa na kina cha mikono kumi kuanzia mbele ya nyumba.

4 Aliitengenezea nyumba hiyo madirisha yenye viunzi ambavyo ukubwa wake ulipungua kutoka nje kwenda ndani.+ 5 Pia, alijenga jengo la kando lililokaribiana na ukuta wa nyumba hiyo; jengo hilo lilizunguka kuta za nyumba hiyo, kuta za hekalu* na za chumba cha ndani zaidi,+ naye akajenga vyumba vya pembeni kuzunguka pande zote.+ 6 Ghorofa ya chini ya vyumba hivyo vya pembeni ilikuwa na upana wa mikono mitano, ghorofa ya katikati ilikuwa na upana wa mikono sita, na ghorofa ya tatu ilikuwa na upana wa mikono saba, kwa maana aliacha sehemu zilizoingia ndani ukutani kuzunguka nyumba yote, ili kitu chochote kisifungwe kwenye kuta za nyumba hiyo.+

7 Nyumba hiyo ilijengwa kwa mawe ya machimboni ambayo tayari yalikuwa yamechongwa,+ hivi kwamba hakuna nyundo wala mashoka wala kifaa chochote cha chuma kilichosikika katika nyumba hiyo ilipokuwa ikijengwa. 8 Mlango wa ghorofa ya chini ulikuwa upande wa kusini* wa nyumba hiyo,+ na ngazi iliyopindapinda ilielekea kwenye ghorofa ya katikati, na kutoka ghorofa ya katikati mpaka ghorofa ya tatu. 9 Aliendelea kujenga nyumba hiyo na kuikamilisha,+ akaifunika nyumba hiyo kwa maboriti ya mierezi na safu za mbao za mierezi.+ 10 Alijenga vyumba vya pembeni kuizunguka,+ kila chumba kilikuwa na kimo cha mikono mitano, navyo viliunganishwa kwenye nyumba hiyo kwa mbao za mierezi.

11 Wakati huo, neno hili la Yehova lilimjia Sulemani: 12 “Kuhusu nyumba hii unayojenga, ikiwa utatembea katika maagizo yangu na kutekeleza sheria zangu* na kushika amri zangu zote kwa kuzifuata,+ mimi pia nitakutimizia ahadi yangu niliyomwahidi baba yako Daudi,+ 13 nami nitakaa miongoni mwa Waisraeli,+ nami sitawaacha watu wangu Waisraeli.”+

14 Sulemani akaendelea kujenga nyumba hiyo ili aikamilishe. 15 Alijenga kuta za ndani za nyumba hiyo kwa mbao za mierezi. Alifunika kuta za ndani kwa mbao, kuanzia sakafu ya nyumba mpaka kwenye maboriti ya dari, akaifunika sakafu yake kwa mbao za miberoshi.+ 16 Na upande wa nyuma wa nyumba hiyo alijenga sehemu fulani yenye ukubwa wa mikono 20 kwa mbao za mierezi, kuanzia sakafuni mpaka kwenye maboriti, na ndani yake* akajenga chumba cha ndani zaidi,+ yaani, Patakatifu Zaidi.+ 17 Na hekalu*+—sehemu ya nyumba iliyokuwa mbele ya Patakatifu Zaidi—lilikuwa mikono 40. 18 Mbao za mierezi zilizokuwa ndani ya nyumba hiyo zilikuwa na michongo ya vibuyu+ na maua yaliyochanua.+ Sehemu yote ilifunikwa kwa mbao za mierezi; hakuna jiwe ambalo lilionekana.

19 Naye akatayarisha chumba cha ndani zaidi+ katika nyumba hiyo ili kuweka humo sanduku la agano la Yehova.+ 20 Chumba hicho cha ndani zaidi kilikuwa na urefu wa mikono 20, upana wa mikono 20, na kimo cha mikono 20;+ naye akakifunika kwa dhahabu safi; akaifunika madhabahu+ kwa mbao za mierezi. 21 Sulemani aliifunika sehemu ya ndani ya nyumba hiyo kwa dhahabu safi,+ naye akaweka minyororo ya dhahabu kutoka upande mmoja hadi mwingine mbele ya chumba hicho cha ndani zaidi+ kilichokuwa kimefunikwa kwa dhahabu. 22 Aliifunika nyumba yote kwa dhahabu mpaka nyumba yote ilipokamilika; pia aliifunika kwa dhahabu madhabahu yote+ iliyokuwa karibu na chumba cha ndani zaidi.

23 Katika chumba cha ndani zaidi alitengeneza makerubi wawili+ kwa mbao za msonobari,* kila kerubi alikuwa na kimo cha mikono kumi.+ 24 Bawa moja la kerubi lilikuwa na urefu wa mikono mitano, na bawa lingine lilikuwa na urefu wa mikono mitano. Urefu kutoka ncha ya bawa moja mpaka ncha ya bawa lingine ulikuwa mikono kumi. 25 Kerubi wa pili alikuwa pia na kimo cha mikono kumi. Makerubi wote wawili walikuwa na ukubwa uleule na umbo lilelile. 26 Kimo cha kerubi mmoja kilikuwa mikono kumi, sawa na kimo cha kerubi wa pili. 27 Kisha akawaweka makerubi+ hao ndani ya chumba cha ndani zaidi cha nyumba hiyo.* Mabawa ya makerubi hao yalikunjuliwa hivi kwamba bawa la kerubi moja lilifika kwenye ukuta mmoja na bawa la kerubi mwingine lilifika kwenye ukuta wa pili, na mabawa yao yalipanuka kuelekea katikati ya nyumba hiyo, hivi kwamba yaligusana. 28 Naye aliwafunika makerubi hao kwa dhahabu.

29 Na kwenye kuta zote kuzunguka nyumba hiyo katika vyumba vyote vya ndani na vya nje, alichonga makerubi,+ mitende,+ na maua yaliyochanua.+ 30 Aliifunika sakafu ya nyumba hiyo kwa dhahabu katika vyumba vya ndani na vya nje. 31 Na aliitengeneza milango ya chumba cha ndani zaidi kwa mbao za msonobari, na pia nguzo za pembeni, na miimo yake, ikiwa sehemu ya tano.* 32 Alitengeneza milango hiyo miwili kwa mbao za msonobari, na kwenye milango hiyo alichonga makerubi, mitende, na maua yaliyochanua, kisha akaifunika kwa dhahabu; akawafunika makerubi hao na mitende hiyo kwa dhahabu akitumia nyundo. 33 Hivyo ndivyo alivyotengeneza miimo ya mlango wa hekalu* iliyokuwa ya mbao za msonobari, zilikuwa sehemu ya nne.* 34 Naye alitengeneza milango miwili kwa mbao za mberoshi. Mlango mmoja ulikuwa na bawaba mbili ambazo zilizunguka kwenye maegemeo, na mlango mwingine ulikuwa na bawaba mbili ambazo zilizunguka kwenye maegemeo.+ 35 Alichonga makerubi, mitende, na maua yaliyochanua, na kufunika michongo hiyo kwa bamba jembamba la dhahabu.

36 Alijenga ua wa ndani+ kwa safu tatu za mawe yaliyochongwa na safu ya maboriti ya mierezi.+

37 Katika mwaka wa nne, mwezi wa Zivu,* msingi wa nyumba ya Yehova ulijengwa;+ 38 na katika mwaka wa 11, mwezi wa Buli,* (yaani, mwezi wa nane), kila kitu katika nyumba hiyo kilikamilishwa kulingana na ramani yake.+ Basi aliijenga kwa miaka saba.

7 Sulemani alijenga nyumba yake mwenyewe*+ kwa miaka 13, mpaka alipoikamilisha nyumba yake yote.+

2 Naye alijenga Nyumba ya Msitu wa Lebanoni+ yenye urefu wa mikono 100,* upana wa mikono 50, na kimo cha mikono 30 juu ya safu nne za nguzo za mierezi; na boriti za mierezi+ zilikuwa juu ya nguzo hizo. 3 Nayo ilifunikwa juu kwa mbao za mierezi zilizokuwa juu ya mihimili iliyolala juu ya nguzo hizo; mihimili hiyo ilikuwa 45, kila safu ilikuwa na mihimili 15. 4 Kulikuwa na safu tatu za madirisha yenye viunzi, na kila dirisha lilielekeana na dirisha lingine katika mistari mitatu. 5 Milango yote na miimo ya milango ilikuwa na viunzi vya mraba,* na sehemu ya mbele ya madirisha yaliyoelekeana katika mistari mitatu ilikuwa pia ya mraba.

6 Naye alijenga Ukumbi wa Nguzo wenye urefu wa mikono 50 na upana wa mikono 30, na mbele yake kulikuwa na ukumbi mwingine wenye nguzo na paa dogo lililochomoza mbele.

7 Alijenga pia Ukumbi wa Kiti cha Ufalme+ ambamo alisikiliza kesi—Ukumbi wa Hukumu+—nao waliufunika kwa mbao za mierezi kuanzia sakafuni mpaka kwenye maboriti.

8 Nyumba* ambamo angeishi, katika ule ua mwingine,+ ilijengwa nyuma mbali na Ukumbi,* na muundo wake ulifanana na wa majengo mengine. Alimjengea pia binti ya Farao nyumba iliyofanana na Ukumbi huo; Sulemani alikuwa amemwoa binti huyo.+

9 Majengo hayo yote yalijengwa kwa mawe ghali+ yaliyochongwa kwa vipimo, yaliyokatwa ndani na nje kwa misumeno ya mawe, kuanzia kwenye msingi mpaka juu ya ukuta, na upande wa nje mpaka kwenye ule ua mkuu.+ 10 Na msingi ulijengwa kwa mawe makubwa sana na yaliyo ghali; baadhi ya mawe yalikuwa na ukubwa wa mikono kumi, na mawe mengine mikono minane. 11 Na juu ya mawe hayo kulikuwa na mawe ghali, yaliyochongwa kwa vipimo, na pia mbao za mierezi. 12 Ua mkuu ulizungukwa na ukuta wenye safu tatu za mawe yaliyochongwa na safu ya maboriti ya mierezi, kama ulivyokuwa ua wa ndani+ wa nyumba ya Yehova na ukumbi wa nyumba.+

13 Mfalme Sulemani akawatuma watu wamwite Hiramu,+ akaletwa kutoka Tiro. 14 Alikuwa mwana wa mwanamke mjane kutoka katika kabila la Naftali, na baba yake alikuwa mfua shaba+ kutoka Tiro; Hiramu alikuwa na ustadi wa hali ya juu, uelewaji,+ na uzoefu wa kutengeneza vitu vya shaba vya kila aina. Basi akaja kwa Mfalme Sulemani na kufanya kazi yake yote.

15 Alitengeneza nguzo mbili kwa kutumia shaba iliyoyeyushwa;+ kila nguzo ilikuwa na urefu wa mikono 18, na kila moja ya nguzo hizo mbili ingeweza kuzungukwa kwa kamba yenye urefu wa mikono 12.*+ 16 Naye alitumia shaba iliyoyeyushwa kutengeneza vifuniko viwili ambavyo vingewekwa juu ya nguzo hizo. Kifuniko kimoja kilikuwa na urefu wa mikono mitano, na kingine kilikuwa na urefu wa mikono mitano. 17 Kifuniko cha kila nguzo kilikuwa na wavu uliofumwa wa minyororo;+ nguzo moja ilikuwa na nyavu saba na nguzo nyingine nyavu saba. 18 Naye alitengeneza safu mbili za makomamanga kuzunguka wavu uliofunika vifuniko vilivyokuwa juu ya nguzo; alifanya hivyo kwa kila nguzo. 19 Vifuniko vilivyokuwa juu ya nguzo za ukumbi vilikuwa na umbo la yungiyungi, na urefu wake ulikuwa mikono minne. 20 Vifuniko hivyo vilikuwa juu ya zile nguzo mbili, juu tu ya sehemu ya mviringo iliyoungana na zile nyavu; na kulikuwa na safu za makomamanga 200 kuzunguka kila kifuniko cha nguzo.+

21 Alisimamisha nguzo za ukumbi wa hekalu.*+ Alisimamisha nguzo ya kulia* na kuiita Yakini,* kisha akasimamisha nguzo ya kushoto* na kuiita Boazi.*+ 22 Sehemu ya juu ya nguzo hizo ilikuwa na umbo la yungiyungi. Basi kazi ya kutengeneza nguzo ikakamilika.

23 Kisha akatengeneza Bahari* kwa madini yaliyoyeyushwa.+ Ilikuwa ya mviringo, yenye upana wa mikono 10 ukingo hadi ukingo na kimo cha mikono 5, na ingeweza kuzungukwa na kamba yenye urefu wa mikono 30.*+ 24 Na chini ya ukingo wake kulikuwa na mapambo ya vibuyu,+ nayo yalizunguka ukingo wote, vibuyu kumi kwa kila mkono mmoja kuzunguka Bahari yote, na safu mbili za vibuyu zilitengenezwa kwa kuyeyushwa zikiwa sehemu ya Bahari hiyo. 25 Ilikuwa juu ya ng’ombe dume 12,+ watatu wakitazama kaskazini, watatu wakitazama magharibi, watatu wakitazama kusini, na watatu wakitazama mashariki; na Bahari hiyo ilikuwa juu yao, na sehemu zao zote za nyuma zilielekea katikati. 26 Na unene wake ulikuwa upana wa kiganja kimoja;* na ukingo wake ulitengenezwa kama ukingo wa kikombe, kama ua la yungiyungi. Ingeweza kujaa maji kiasi cha bathi 2,000.*

27 Kisha akatengeneza magari kumi*+ ya shaba. Kila gari lilikuwa na urefu wa mikono minne, upana wa mikono minne, na kimo cha mikono mitatu. 28 Na hivi ndivyo magari hayo yalivyotengenezwa: Yalikuwa na kuta za pembeni, na kuta hizo za pembeni zilikuwa kati ya mihimili. 29 Na kwenye kuta hizo za pembeni kati ya mihimili hiyo kulikuwa na simba,+ ng’ombe dume, na makerubi,+ na muundo huohuo ulikuwa kwenye mihimili. Juu na chini ya simba na ng’ombe dume hao kulikuwa na mashada ya maua yaliyoyeyushwa. 30 Na kila gari lilikuwa na magurudumu manne ya shaba na vyuma vya katikati vya shaba vinavyozungusha magurudumu hayo, na nguzo nne za pembeni ziliyashikilia. Na kila upande chini ya beseni kulikuwa na vitegemezo vilivyotengenezwa kwa mashada ya maua yaliyoyeyushwa. 31 Mdomo wake ulikuwa katika sehemu ya juu, nao ulichomoza juu kwa kipimo cha mkono mmoja; na mdomo huo ulikuwa wa mviringo, na kitako chote kilikuwa na urefu wa mkono mmoja na nusu, na mdomo wake ulikuwa na michongo. Na kuta za pembeni za magari hayo zilikuwa za mraba, si mviringo. 32 Na yale magurudumu manne yalikuwa chini ya kuta hizo, na nguzo zilizoshikilia magurudumu ziliunganishwa na gari, na kila gurudumu lilikuwa na kimo cha mkono mmoja na nusu. 33 Na magurudumu hayo yalitengenezwa kama magurudumu ya gari la vita. Nguzo zake, mizingo yake, njukuti,* na vitovu vya magudurumu, vyote vilitengenezwa kwa kuyeyushwa. 34 Kulikuwa na nguzo nne kwenye pembe nne za kila gari; nguzo hizo zilitengenezwa kwa kuyeyushwa zikiwa sehemu ya gari hilo.* 35 Juu ya gari hilo kulikuwa na utepe wa mviringo wenye kimo cha nusu mkono, na viunzi vyake na kuta zake za pembeni zilikuwa juu ya gari hilo, nazo zilitengenezwa kwa kuyeyushwa zikiwa sehemu ya gari hilo.* 36 Juu ya viunzi vyake na kwenye kuta zake za pembeni alichonga makerubi, simba, na mitende kulingana na nafasi iliyopatikana kwenye kila kipande, na mashada ya maua kuzunguka pande zote.+ 37 Hivyo ndivyo alivyoyatengeneza magari hayo kumi;+ yote yalitengenezwa kwa kuyeyushwa kwa njia ileile,+ yakiwa na vipimo na umbo lilelile.

38 Alitengeneza mabeseni kumi ya shaba;+ kila beseni lingeweza kujaa kiasi cha bathi 40 za maji. Kila beseni lilikuwa na upana wa mikono 4.* Kulikuwa na beseni moja kwa ajili ya kila mojawapo ya magari hayo kumi. 39 Kisha akaweka magari matano upande wa kulia wa nyumba, na matano upande wa kushoto wa nyumba; akaiweka ile Bahari upande wa kulia wa nyumba, kuelekea kusini mashariki.+

40 Hiramu+ alitengeneza pia mabeseni, sepetu,+ na mabakuli.+ Basi Hiramu akamaliza kazi yote aliyomfanyia Mfalme Sulemani kuhusiana na nyumba ya Yehova:+ 41 zile nguzo mbili+ na vifuniko vyenye umbo la bakuli vilivyokuwa juu ya nguzo hizo; na nyavu mbili+ za kufunika vifuniko hivyo viwili vyenye umbo la bakuli vilivyokuwa juu ya nguzo hizo; 42 yale makomamanga 400+ kwa ajili ya zile nyavu mbili, safu mbili za makomamanga kwa ajili ya kila wavu, ili kufunika vile vifuniko viwili vyenye umbo la bakuli vilivyokuwa juu ya zile nguzo mbili; 43 yale magari kumi+ na yale mabeseni kumi+ yaliyokuwa juu ya magari hayo; 44 ile Bahari+ na wale ng’ombe dume 12 waliokuwa chini ya Bahari hiyo; 45 na ndoo za kuondolea majivu, sepetu, mabakuli, na vyombo vyote ambavyo Hiramu alimtengenezea Mfalme Sulemani kwa shaba iliyong’arishwa kwa ajili ya nyumba ya Yehova. 46 Mfalme alivitengeneza katika kalibu za udongo wa mfinyanzi katika wilaya ya Yordani, kati ya Sukothi na Sarethani.

47 Sulemani hakupima uzito wa chombo chochote kwa sababu vyombo hivyo vilikuwa vingi sana. Uzito wa shaba haukujulikana.+ 48 Sulemani alivitengeneza vitu vyote vya nyumba ya Yehova: madhabahu+ ya dhahabu; meza ya dhahabu+ ya kuwekea mikate ya wonyesho; 49 vinara vya taa+ vya dhahabu safi, vitano upande wa kulia na vitano upande wa kushoto mbele ya chumba cha ndani zaidi; na maua,+ taa, na koleo, vyote vya dhahabu;+ 50 mabeseni, mikasi ya kukatia tambi za taa,+ mabakuli, vikombe,+ na vyetezo,+ vyote vya dhahabu safi; na bawaba za milango ya nyumba ya ndani,+ yaani, Patakatifu Zaidi, na za milango ya nyumba ya hekalu,+ vyote vya dhahabu.

51 Kwa hiyo Mfalme Sulemani akakamilisha kazi yote aliyopaswa kufanya kwa ajili ya nyumba ya Yehova. Kisha Sulemani akaingiza ndani vitu ambavyo Daudi baba yake alikuwa amevifanya kuwa vitakatifu,+ naye akaweka fedha, dhahabu, na vitu hivyo katika hazina za nyumba ya Yehova.+

8 Wakati huo Sulemani aliwakusanya+ wazee wa Israeli—viongozi wote wa makabila, wakuu wa koo* za Israeli.+ Wakaja kwa Mfalme Sulemani huko Yerusalemu ili kuliondoa sanduku la agano la Yehova katika Jiji la Daudi,+ yaani, Sayuni.+ 2 Wanaume wote wa Israeli wakakusanyika mbele ya Mfalme Sulemani wakati wa sherehe* katika mwezi wa Ethanimu,* yaani, mwezi wa saba.+ 3 Basi wazee wote wa Israeli wakaja, na makuhani wakalibeba Sanduku.+ 4 Wakalipandisha kutoka huko Sanduku la Yehova, hema la mkutano,+ na vyombo vyote vitakatifu vilivyokuwa katika hema hilo. Makuhani na Walawi wakavipandisha vitu hivyo. 5 Mfalme Sulemani na Waisraeli wote waliokusanywa ili wakutane naye, walikuwa mbele ya Sanduku. Kondoo na ng’ombe wengi sana wasiohesabika au kujulikana idadi walikuwa wakitolewa dhabihu.+

6 Kisha makuhani wakalileta sanduku la agano la Yehova mahali pake,+ katika chumba cha ndani zaidi cha nyumba, yaani, Patakatifu Zaidi, chini ya mabawa ya makerubi.+

7 Kwa hiyo mabawa ya makerubi yalikuwa yamenyooshwa juu ya mahali ambapo Sanduku liliwekwa, hivi kwamba makerubi hao walilifunika Sanduku na fito zake.+ 8 Fito hizo+ zilikuwa ndefu sana hivi kwamba ncha zake zilionekana kutoka Patakatifu mbele ya chumba cha ndani zaidi, lakini hazikuonekana kutoka upande wa nje. Nazo ziko huko mpaka leo hii. 9 Hakukuwa na kitu kingine ndani ya Sanduku hilo isipokuwa yale mabamba mawili ya mawe+ ambayo Musa aliyaweka humo+ kule Horebu, Yehova alipofanya agano+ na Waisraeli walipokuwa wakitoka nchini Misri.+

10 Makuhani walipotoka mahali patakatifu, wingu+ lilijaa katika nyumba ya Yehova.+ 11 Makuhani hawakuweza kusimama ili kuhudumu kwa sababu ya wingu hilo, kwa maana utukufu wa Yehova ulijaa katika nyumba ya Yehova.+ 12 Wakati huo Sulemani akasema: “Yehova alisema kwamba atakaa katika giza zito.+ 13 Nimefanikiwa kukujengea nyumba iliyokwezwa, mahali palipofanywa imara ili ukae humo milele.”+

14 Kisha mfalme akageuka na kuanza kulibariki kutaniko lote la Waisraeli huku kutaniko lote la Waisraeli likiwa limesimama.+ 15 Akasema: “Na asifiwe Yehova Mungu wa Israeli, ambaye kwa kinywa chake mwenyewe alimwahidi baba yangu Daudi, na kwa mkono wake mwenyewe ametimiza, akisema, 16 ‘Kuanzia siku niliyowatoa watu wangu Waisraeli nchini Misri, sijachagua jiji katika makabila yote ya Israeli na kujenga humo nyumba ili jina langu likae humo,+ lakini nimemchagua Daudi awatawale watu wangu Waisraeli.’ 17 Moyo wa baba yangu Daudi ulitamani kujenga nyumba kwa ajili ya jina la Yehova Mungu wa Israeli.+ 18 Lakini Yehova akamwambia Daudi baba yangu, ‘Moyo wako ulitamani kujenga nyumba kwa ajili ya jina langu, na ulifanya vizuri kutamani jambo hilo moyoni mwako. 19 Hata hivyo, hutajenga nyumba hiyo, lakini mwana wako mwenyewe utakayemzaa* ndiye atakayeijenga nyumba hiyo kwa ajili ya jina langu.’+ 20 Yehova ametimiza ahadi hiyo aliyoitoa, kwa maana nimechukua mahali pa baba yangu Daudi na kuketi kwenye kiti cha ufalme cha Israeli, kama Yehova alivyoahidi. Pia nimejenga nyumba kwa ajili ya jina la Yehova Mungu wa Israeli,+ 21 nami nimetenga mahali humo kwa ajili ya lile Sanduku lenye agano+ ambalo Yehova alifanya na mababu zetu alipokuwa akiwatoa nchini Misri.”

22 Kisha Sulemani akasimama mbele ya madhabahu ya Yehova mbele ya kutaniko lote la Waisraeli, akanyoosha mikono yake kuelekea mbinguni,+ 23 akasema: “Ee Yehova Mungu wa Israeli, hakuna Mungu kama wewe+ juu mbinguni wala chini duniani, unayeshika agano na kuwatendea kwa upendo mshikamanifu+ watumishi wako wanaotembea mbele zako kwa moyo wao wote.+ 24 Umetimiza ahadi uliyomwahidi mtumishi wako Daudi baba yangu. Ulitoa ahadi hiyo kwa kinywa chako mwenyewe, na siku ya leo umeitimiza kwa mkono wako mwenyewe.+ 25 Na sasa, Ee Yehova Mungu wa Israeli, timiza ahadi uliyomwahidi mtumishi wako Daudi baba yangu ulipomwambia, ‘Hutakosa kamwe mwanamume wa uzao wako atakayeketi kwenye kiti cha ufalme cha Israeli mbele zangu, ikiwa tu wana wako watakazia uangalifu njia yao kwa kutembea mbele zangu, kama ulivyotembea mbele zangu.’+ 26 Na sasa, Ee Mungu wa Israeli, tafadhali acha ahadi uliyomwahidi mtumishi wako Daudi baba yangu ithibitike kuwa ya kweli.

27 “Lakini Ee Mungu, je, kweli utakaa duniani?+ Tazama! Mbingu, naam, mbingu za mbingu, haziwezi kukutosha;+ sembuse nyumba hii niliyoijenga!+ 28 Sasa sikiliza sala yangu mimi mtumishi wako na ombi langu la kutaka kibali, Ee Yehova Mungu wangu, sikiliza kilio changu cha kuomba msaada na sala ambayo mimi mtumishi wako ninasali leo mbele zako. 29 Macho yako na yatazame nyumba hii usiku na mchana, yatazame mahali ambapo ulisema hivi kupahusu: ‘Jina langu litakuwa hapo,’+ ili usikilize sala ambayo mimi mtumishi wako ninasali kuelekea mahali hapa.+ 30 Nawe usikilize ombi langu mimi mtumishi wako la kutaka kibali na pia ombi ambalo watu wako Waisraeli wanaomba kuelekea mahali hapa, nawe usikilize katika makao yako mbinguni;+ naam, usikilize na kusamehe.+

31 “Mwanadamu akimtendea dhambi mwanadamu mwenzake, naye aapishwe* na kuwekwa chini ya wajibu wa kiapo hicho,* naye akiwa chini ya kiapo* aje mbele ya madhabahu yako katika nyumba hii,+ 32 basi usikie kutoka mbinguni na kuchukua hatua na kuwahukumu watumishi wako kwa kumtangaza yule mwovu kuwa na hatia na kumwadhibu kwa sababu ya jambo alilotenda,* na kumtangaza mwadilifu kuwa asiye na hatia* na kumthawabisha kulingana na uadilifu wake mwenyewe.+

33 “Watu wako Waisraeli wakishindwa na maadui kwa sababu ya kuzidi kukutendea dhambi,+ nao warudi kwako na kulitukuza jina lako+ na kusali na kukusihi wapate kibali katika nyumba hii,+ 34 basi usikie kutoka mbinguni na kuwasamehe watu wako Waisraeli dhambi yao na kuwarudisha katika nchi uliyowapa mababu zao.+

35 “Mbingu zikifungwa kusiwe na mvua+ kwa sababu wamezidi kukutendea dhambi,+ nao wasali kuelekea mahali hapa na kulitukuza jina lako na kuacha dhambi yao kwa sababu umewanyenyekeza,*+ 36 basi usikie kutoka mbinguni na kuwasamehe watumishi wako dhambi yao, dhambi ya watu wako Waisraeli, kwa sababu utawafundisha+ njia nzuri wanayopaswa kufuata; na ulete mvua katika nchi yako+ ambayo uliwapa watu wako kuwa urithi.

37 “Njaa kali ikitokea nchini,+ au ugonjwa hatari, upepo unaochoma, kuvu,+ makundi ya nzige, au parare* wanaokula sana; au maadui wao wakiwazingira katika jiji lolote nchini* au pigo au ugonjwa wa aina yoyote ukitokea,+ 38 sala yoyote, ombi lolote la kutaka kibali+ ambalo huenda likatolewa na mtu yeyote au na watu wako wote Waisraeli (kwa sababu kila mmoja anajua mateso yaliyo katika moyo wake mwenyewe)+ wakinyoosha mikono yao kuelekea nyumba hii, 39 basi usikie kutoka mbinguni, makao yako,+ nawe usamehe+ na kuchukua hatua; na umthawabishe kila mmoja kulingana na njia zake zote,+ kwa sababu unajua moyo wake (ni wewe peke yako unayejua vizuri moyo wa kila mwanadamu),+ 40 ili wakuogope sikuzote watakazoishi katika nchi uliyowapa mababu zetu.

41 “Pia mgeni ambaye si sehemu ya watu wako Waisraeli na ambaye anatoka katika nchi ya mbali kwa sababu ya jina lako*+ 42 (kwa maana watasikia kuhusu jina lako kuu+ na mkono wako wenye nguvu na mkono wako ulionyooshwa), akija na kusali kuelekea nyumba hii, 43 basi usikilize kutoka mbinguni, makao yako,+ nawe ufanye mambo yote ambayo mgeni huyo anakuomba ufanye, ili watu wote duniani wajue jina lako na kukuogopa,+ kama watu wako Waisraeli wanavyokuogopa, na ili wajue kwamba nyumba hii niliyojenga imeitwa kwa jina lako.

44 “Watu wako wakienda vitani kupigana na maadui wao mahali utakapowaelekeza,+ nao wasali+ kwako wewe, Yehova, kuelekea jiji ambalo umechagua+ na kuelekea nyumba ambayo nimejenga kwa ajili ya jina lako,+ 45 basi usikie kutoka mbinguni sala yao na ombi lao la kutaka kibali, nawe utekeleze hukumu kwa ajili yao.

46 “Wakikutendea dhambi (kwa sababu hakuna mwanadamu asiyetenda dhambi),+ nawe uwakasirikie vikali na kuwaacha mikononi mwa maadui, na waliowateka wawapeleke katika nchi ya maadui, mbali au karibu;+ 47 nao warudiwe na ufahamu wakiwa katika nchi ya watu waliowachukua mateka,+ na kukurudia+ na kuomba kibali chako wakisema, ‘Tumetenda dhambi na kukosea; tumetenda uovu,’+ 48 nao wakurudie kwa moyo wao wote+ na kwa nafsi* yao yote katika nchi ya maadui wao waliowachukua mateka, nao wasali kwako kuelekea nchi yao ambayo uliwapa mababu zao na kuelekea jiji ambalo umelichagua na nyumba ambayo nimejenga kwa ajili ya jina lako,+ 49 basi usikie kutoka mbinguni, makao yako,+ sala yao na ombi lao la kutaka kibali, nawe utekeleze hukumu kwa ajili yao 50 na uwasamehe watu wako ambao wamekutendea dhambi, na kusamehe makosa yote waliyokukosea. Utafanya waliowateka wawahurumie,* nao watawahurumia+ 51 (kwa maana wao ni watu wako na urithi wako,+ uliowatoa Misri,+ kutoka ndani ya tanuru la kuyeyushia chuma).+ 52 Macho yako yatazame ombi langu mimi mtumishi wako la kutaka kibali+ na ombi la kutaka kibali la watu wako Waisraeli kwa kuwasikiliza wakati wowote wanapokulilia.*+ 53 Kwa maana uliwatenga wawe urithi wako kutoka kati ya mataifa yote ya dunia,+ kama ulivyotangaza kupitia mtumishi wako Musa ulipokuwa ukiwatoa mababu zetu Misri, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”

54 Mara tu Sulemani alipomaliza kumtolea Yehova sala hiyo yote na kuomba kibali chake, aliinuka kutoka mbele ya madhabahu ya Yehova, mahali alipokuwa amepiga magoti akiwa amenyoosha mikono yake kuelekea mbinguni.+ 55 Kisha akasimama na kulibariki kwa sauti kubwa kutaniko lote la Waisraeli akisema: 56 “Na asifiwe Yehova, ambaye amewapa watu wake Waisraeli mahali pa kupumzikia, kama alivyoahidi.+ Hakuna ahadi yoyote kati ya ahadi zake zote nzuri ambazo aliahidi kupitia Musa mtumishi wake iliyokosa kutimia.+ 57 Yehova Mungu wetu na awe pamoja nasi kama tu alivyokuwa pamoja na mababu zetu.+ Naye asituache wala kututupa.+ 58 Na aivute mioyo yetu kwake+ ili tutembee katika njia zake zote na kushika amri zake, masharti yake, na sheria zake,* ambazo aliwaamuru mababu zetu washike. 59 Na maneno haya yangu ambayo nimesema ili kumwomba Yehova kibali na yawe karibu na Yehova Mungu wetu mchana na usiku, ili atekeleze hukumu kwa ajili yangu mimi mtumishi wake na kwa ajili ya watu wake Waisraeli kulingana na mahitaji ya kila siku, 60 ili mataifa yote duniani yajue kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli.+ Hakuna mwingine!+ 61 Basi acheni mioyo yenu iwe kamili+ kwa* Yehova Mungu wetu kwa kufuata masharti yake na kushika amri zake kama ilivyo leo.”

62 Kisha mfalme na Waisraeli wote wakamtolea Yehova dhabihu kubwa.+ 63 Sulemani alimtolea Yehova dhabihu za ushirika:+ Alitoa ng’ombe 22,000 na kondoo 120,000. Basi mfalme na Waisraeli wote wakaizindua nyumba ya Yehova.+ 64 Siku hiyo ilimbidi mfalme atakase sehemu ya katikati ya ua ulio mbele ya nyumba ya Yehova, kwa sababu alipaswa kutolea mahali hapo dhabihu za kuteketezwa, matoleo ya nafaka, na vipande vya mafuta vya dhabihu za ushirika, kwa sababu madhabahu ya shaba+ iliyo mbele za Yehova ilikuwa ndogo sana isiweze kutoshea dhabihu za kuteketezwa, matoleo ya nafaka, na vipande vya mafuta+ vya dhabihu za ushirika. 65 Wakati huo Sulemani alifanya sherehe hiyo+ pamoja na Waisraeli wote, kutaniko kubwa kuanzia Lebo-hamathi* na kushuka mpaka kwenye Korongo* la Misri,+ mbele za Yehova Mungu wetu kwa siku 7 na kisha siku nyingine 7, jumla ya siku 14. 66 Siku iliyofuata,* aliwaruhusu watu waondoke, nao wakambariki mfalme na kwenda nyumbani kwao wakishangilia na kufurahi moyoni kwa sababu ya wema wote+ ambao Yehova alikuwa amemtendea Daudi mtumishi wake na watu wake Waisraeli.

9 Mara tu Sulemani alipomaliza kujenga nyumba ya Yehova, nyumba ya mfalme,*+ na kila kitu ambacho Sulemani alitamani kufanya,+ 2 Yehova akamtokea Sulemani mara ya pili, kama alivyokuwa amemtokea kule Gibeoni.+ 3 Yehova akamwambia: “Nimesikia sala yako na ombi lako la kutaka kibali ulilotoa mbele zangu. Nimeitakasa nyumba hii ambayo umejenga kwa kuliweka jina langu humu milele,+ na macho yangu na moyo wangu utakuwa humu sikuzote.+ 4 Nawe, ikiwa utatembea mbele zangu kama Daudi baba yako alivyotembea,+ kwa utimilifu wa moyo+ na kwa unyoofu,+ kwa kutenda mambo yote niliyokuamuru,+ nawe ukitii masharti yangu na sheria* zangu,+ 5 ndipo nitakapoimarisha kiti chako cha ufalme juu ya Israeli milele, kama nilivyomwahidi Daudi baba yako, kwa kusema, ‘Hutakosa kamwe mwanamume wa uzao wako atakayeketi kwenye kiti cha ufalme cha Israeli.’+ 6 Lakini ikiwa ninyi na wana wenu mtageuka na kuacha kunifuata na kuacha kushika amri zangu na maagizo yangu ambayo nimeweka mbele yenu, nanyi mwende na kuabudu miungu mingine na kuiinamia,+ 7 nitawaondolea mbali Waisraeli kutoka katika nchi ambayo nimewapa,+ na nyumba ambayo nimeitakasa kwa ajili ya jina langu nitaitupilia mbali kutoka mbele za macho yangu,+ na Israeli itakuwa kitu cha kudharauliwa* na kitu cha kudhihakiwa miongoni mwa mataifa yote.+ 8 Na nyumba hii itakuwa marundo ya magofu.+ Kila mtu atakayepita karibu nayo ataitazama kwa mshangao, atapiga mluzi na kuuliza, ‘Kwa nini Yehova aliitendea hivi nchi hii na nyumba hii?’+ 9 Kisha watasema, ‘Ni kwa sababu walimwacha Yehova Mungu wao, aliyewatoa mababu zao kutoka nchini Misri, nao wakashikamana na miungu mingine, wakaiinamia na kuiabudu. Ndiyo sababu Yehova aliwaletea msiba huo wote.’”+

10 Katika muda wa miaka 20 ambayo Sulemani alijenga nyumba hizo mbili, yaani, nyumba ya Yehova na nyumba ya* mfalme,+ 11 Hiramu+ mfalme wa Tiro alimpa Sulemani mbao za mierezi na mbao za miberoshi na dhahabu nyingi sana kadiri alivyohitaji,+ naye Mfalme Sulemani akampa Hiramu majiji 20 katika nchi ya Galilaya. 12 Basi Hiramu akatoka Tiro kwenda kuyaona majiji ambayo Sulemani alikuwa amempa, lakini hakuridhika nayo.* 13 Akamuuliza: “Ndugu yangu, ni majiji gani haya ambayo umenipa?” Basi tangu siku hiyo yakaitwa Nchi ya Kabuli.* 14 Wakati huo, Hiramu akamtumia mfalme talanta 120* za dhahabu.+

15 Habari ifuatayo inawahusu watu ambao Mfalme Sulemani aliwaandikisha kufanya kazi ya kulazimishwa+ ili wajenge nyumba ya Yehova,+ nyumba yake mwenyewe,* Kilima,*+ ukuta wa Yerusalemu, Hasori,+ Megido,+ na Gezeri.+ 16 (Farao mfalme wa Misri alikuwa amekuja na kuliteka jiji la Gezeri na kuliteketeza kwa moto, na alikuwa pia amewaua Wakanaani+ walioishi katika jiji hilo. Basi akampa binti yake,+ mke wa Sulemani, jiji hilo kama zawadi ya kumuaga.*) 17 Sulemani akalijenga* jiji la Gezeri, Beth-horoni la Chini,+ 18 Baalathi,+ na Tamari lililo nyikani, yaliyokuwa nchini, 19 na pia majiji yote ya Sulemani yenye maghala, majiji ya magari ya vita,+ majiji ya wapanda farasi, na chochote ambacho Sulemani alitamani kujenga huko Yerusalemu, Lebanoni, na katika nchi yote iliyokuwa chini ya mamlaka yake. 20 Watu wengine wote waliobaki miongoni mwa Waamori, Wahiti, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi,+ ambao hawakuwa sehemu ya taifa la Israeli,+ 21 wazao wao waliobaki nchini, ambao Waisraeli walishindwa kuwaangamiza, Sulemani aliwaandikisha ili wafanye kazi ya kulazimishwa kama watumwa mpaka leo hii.+ 22 Lakini Sulemani hakumfanya Mwisraeli yeyote kuwa mtumwa,+ kwa sababu walikuwa mashujaa wake, watumishi, wakuu, makamanda wasaidizi, wakuu wa wale walioendesha magari yake ya vita na wapanda farasi wake. 23 Kulikuwa na wakuu 550 wa wasaidizi waliosimamia kazi ya Sulemani, wasimamizi wa watu waliokuwa wakifanya kazi.+

24 Lakini binti ya Farao+ akatoka katika Jiji la Daudi+ akaenda kuishi katika nyumba yake ambayo Sulemani alimjengea; kisha Sulemani akajenga Kilima.*+

25 Mara tatu kwa mwaka+ Sulemani alitoa dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ushirika kwenye madhabahu aliyomjengea Yehova,+ pia alifukiza moshi wa dhabihu kwenye madhabahu iliyokuwa mbele za Yehova, basi akaikamilisha nyumba.+

26 Mfalme Sulemani akatengeneza pia kundi la meli katika jiji la Esion-geberi,+ lililo kando ya Elothi, ufuoni mwa Bahari Nyekundu katika nchi ya Edomu.+ 27 Hiramu akawatuma watumishi wake mwenyewe, mabaharia wenye uzoefu, wakafanye kazi pamoja na watumishi wa Sulemani kwenye kundi hilo la meli.+ 28 Wakaenda Ofiri,+ wakachukua talanta 420 za dhahabu na kumletea Mfalme Sulemani.

10 Basi malkia wa Sheba alisikia habari za Sulemani kuhusiana na jina la Yehova,+ kwa hiyo akaja kumjaribu kwa maswali magumu.*+ 2 Alifika Yerusalemu na msafara wenye kuvutia sana,+ pamoja na ngamia waliobeba mafuta ya zeri+ na dhahabu nyingi sana na mawe yenye thamani. Akafika mbele ya Sulemani na kumwambia mambo yote yaliyokuwa moyoni mwake. 3 Kisha Sulemani akajibu maswali yake yote. Hakuna jambo lolote lililokuwa gumu sana* kwa mfalme asiweze kumweleza.

4 Malkia wa Sheba alipoona hekima yote ya Sulemani,+ nyumba aliyojenga,+ 5 chakula kilichokuwa mezani pake,+ jinsi watumishi wake walivyoketi, jinsi watumishi wake walivyohudumu mezani na pia mavazi yao, na wale waliompa vinywaji, na dhabihu zake za kuteketezwa alizotoa kwa ukawaida katika nyumba ya Yehova, alipigwa na bumbuazi.* 6 Basi akamwambia mfalme: “Habari nilizosikia katika nchi yangu kuhusu mafanikio* yako na kuhusu hekima yako zilikuwa za kweli. 7 Lakini sikuamini habari hizo mpaka nilipokuja na kujionea kwa macho yangu mwenyewe. Na kwa kweli sikuwa nimeambiwa hata nusu yake. Hekima yako na ufanisi wako umezidi kwa mbali habari nilizosikia. 8 Wenye furaha ni watu wako, na wenye furaha ni watumishi wako wanaosimama mbele yako daima, wakiisikiliza hekima yako!+ 9 Na asifiwe Yehova Mungu wako,+ ambaye amependezwa nawe, akakuweka kwenye kiti cha ufalme cha Israeli. Kwa sababu ya upendo wa milele wa Yehova kwa Waisraeli, alikuweka rasmi kuwa mfalme ili utekeleze haki na uadilifu.”

10 Kisha akampa mfalme talanta 120* za dhahabu na kiasi kikubwa sana cha mafuta ya zeri+ na mawe yenye thamani.+ Mfalme Sulemani hakuwahi tena kuletewa kiasi kikubwa hivyo cha mafuta ya zeri kama alicholetewa na malkia wa Sheba.

11 Kundi la meli za Hiramu zilizobeba dhahabu kutoka Ofiri+ zilileta pia mbao nyingi sana za misandali kutoka Ofiri,+ na mawe yenye thamani.+ 12 Mfalme alitumia mbao hizo za misandali kutengeneza vitegemezi vya nyumba ya Yehova na nyumba ya mfalme,* na pia vinubi na vinanda vya waimbaji.+ Mbao za misandali kama hizo hazijawahi tena kuletwa wala kuonekana mpaka leo hii.

13 Mfalme Sulemani alimpa pia malkia wa Sheba kitu chochote alichotamani na kuomba, mbali na vitu alivyompa kwa ukarimu wake mwenyewe.* Baada ya hayo aliondoka na kurudi katika nchi yake, pamoja na watumishi wake.+

14 Na dhahabu iliyoletwa kwa Sulemani katika mwaka mmoja ilikuwa na uzito wa talanta 666 za dhahabu,+ 15 mbali na dhahabu iliyoletwa na wafanyabiashara wasafiri na pia faida kutoka kwa wauzaji wa bidhaa na kutoka kwa wafalme wote wa Uarabuni na magavana wa nchi.

16 Mfalme Sulemani alitengeneza ngao kubwa 200 za dhahabu iliyochanganywa na madini mengine+ (kwa kila ngao alitumia shekeli 600* za dhahabu)+ 17 na ngao ndogo* 300 za dhahabu iliyochanganywa na madini mengine (kwa kila ngao ndogo alitumia mina tatu* za dhahabu). Kisha mfalme akaziweka katika Nyumba ya Msitu wa Lebanoni.+

18 Mfalme pia alitengeneza kiti kikubwa cha ufalme cha pembe za tembo+ na kukifunika kwa dhahabu safi.+ 19 Kiti hicho cha ufalme kilikuwa na ngazi sita, kilikuwa na kifuniko cha mviringo mgongoni, nacho kilikuwa na mikono pande zote mbili, na simba wawili+ walisimama kando ya mikono hiyo. 20 Na kulikuwa na simba 12 waliosimama kwenye ngazi hizo sita, wawili kwenye kila ngazi, mmoja upande huu na mwingine upande wa pili. Hakuna ufalme mwingine wowote uliokuwa umetengeneza kiti kama hicho.

21 Vyombo vyote vya kunywea vya Mfalme Sulemani vilikuwa vya dhahabu, na vyombo vyote vya Nyumba ya Msitu wa Lebanoni+ vilikuwa vya dhahabu safi. Hakukuwa na kitu chochote kilichotengenezwa kwa fedha, kwa maana fedha ilionwa kuwa si kitu katika siku za Sulemani.+ 22 Mfalme alikuwa na kundi la meli za Tarshishi+ baharini pamoja na kundi la meli za Hiramu. Mara moja baada ya kila miaka mitatu, kundi la meli za Tarshishi zilikuja zikiwa zimejazwa dhahabu na fedha, pembe za tembo,+ sokwe, na tausi.

23 Kwa hiyo Mfalme Sulemani alikuwa na utajiri+ mwingi zaidi na hekima+ kuliko wafalme wengine wote duniani. 24 Na watu wote duniani walitaka kukutana na* Sulemani ili wasikie hekima yake ambayo Mungu alikuwa ameweka moyoni mwake.+ 25 Kila mmoja wao alileta zawadi—vitu vya fedha, vitu vya dhahabu, mavazi, silaha, mafuta ya zeri, farasi, na nyumbu—na walifanya hivyo mwaka baada ya mwaka.

26 Na Sulemani akaendelea kukusanya magari ya vita na farasi;* akawa na magari 1,400 ya vita na farasi* 12,000,+ naye aliwaweka katika majiji ya magari ya vita karibu naye huko Yerusalemu.+

27 Mfalme alifanya fedha huko Yerusalemu iwe nyingi kama mawe, na mbao za mierezi ziwe nyingi kama mikuyu katika Shefela.+

28 Farasi wa Sulemani waliletwa kutoka Misri, na wafanyabiashara wa mfalme walinunua makundi ya farasi* kwa bei moja.+ 29 Kila gari kutoka Misri lilinunuliwa kwa vipande 600 vya fedha, na farasi alinunuliwa kwa vipande 150; kisha waliwauzia wafalme wote wa Wahiti+ na wafalme wa Siria.

11 Lakini mbali na binti ya Farao,+ Mfalme Sulemani aliwapenda wanawake wengi wa kigeni:+ wanawake Wamoabu,+ Waamoni,+ Waedomu, Wasidoni,+ na Wahiti.+ 2 Walitoka katika mataifa ambayo Yehova alikuwa amewaambia hivi Waisraeli kuyahusu: “Hampaswi kuingia miongoni mwao,* nao hawapaswi kuingia miongoni mwenu; kwa maana kwa hakika wataigeuza mioyo yenu ifuate miungu yao.”+ Lakini Sulemani alishikamana nao na kuwapenda. 3 Naye alikuwa na wake 700 waliokuwa mabinti wa wafalme na masuria 300, na hatua kwa hatua wake zake wakaugeuza moyo wake.* 4 Sulemani alipozeeka,+ wake zake waliugeuza* moyo wake ukaifuata miungu mingine,+ na moyo wake haukuwa kamili kwa* Yehova Mungu wake kama moyo wa Daudi baba yake. 5 Na Sulemani akamfuata Ashtorethi,+ mungu wa kike wa Wasidoni, na Milkomu,+ mungu mwenye kuchukiza wa Waamoni. 6 Na Sulemani akatenda maovu machoni pa Yehova, naye hakumfuata Yehova kikamili kama Daudi baba yake alivyomfuata.+

7 Wakati huo ndipo Sulemani alipojenga mahali pa juu+ kwa ajili ya Kemoshi, mungu mwenye kuchukiza wa Moabu, kwenye mlima uliokuwa mbele ya Yerusalemu, na kwa ajili ya Moleki,+ mungu mwenye kuchukiza wa Waamoni.+ 8 Hivyo ndivyo alivyowafanyia wake zake wote wa kigeni waliokuwa wakifukiza moshi wa dhabihu na kuitolea dhabihu miungu yao.

9 Yehova akamkasirikia vikali Sulemani, kwa sababu moyo wake ulikuwa umegeuka na kumwacha Yehova Mungu wa Israeli,+ aliyekuwa amemtokea mara mbili+ 10 na kumwonya kuhusu jambo hilohilo, kwamba hapaswi kuifuata miungu mingine.+ Lakini hakutii amri ya Yehova. 11 Sasa Yehova akamwambia Sulemani: “Kwa sababu umefanya jambo hili, nawe hukushika agano langu na sheria zangu nilizokuamuru, kwa hakika nitaurarua ufalme kutoka kwako, nami nitampa mmoja wa watumishi wako.+ 12 Hata hivyo, kwa ajili ya Daudi baba yako, sitafanya hivyo maishani mwako. Nitaurarua kutoka mikononi mwa mwana wako,+ 13 lakini sitaurarua ufalme wote.+ Kabila moja nitampa mwana wako,+ kwa ajili ya Daudi mtumishi wangu na kwa ajili ya Yerusalemu, jiji ambalo nimechagua.”+

14 Ndipo Yehova akatokeza mtu wa kumpinga Sulemani,+ yaani, Hadadi Mwedomu, wa ukoo wa kifalme wa Edomu.+ 15 Daudi aliposhinda Edomu,+ Yoabu mkuu wa jeshi alipanda kwenda kuwazika waliouawa, naye akajaribu kumuua kila mwanamume huko Edomu. 16 (Kwa maana Yoabu na Waisraeli wote walikaa huko kwa miezi sita mpaka alipokuwa amemwangamiza kila mwanamume huko Edomu.) 17 Lakini Hadadi alikimbia pamoja na baadhi ya Waedomu waliokuwa watumishi wa baba yake, wakaenda Misri; wakati huo Hadadi alikuwa mvulana mdogo. 18 Basi wakaondoka Midiani na kufika Parani. Walichukua wanaume kutoka Parani+ na kwenda Misri, kwa Farao mfalme wa Misri, ambaye alimpa nyumba, akaamuru awe akipewa chakula, na pia akampa ardhi. 19 Hadadi alipata kibali machoni pa Farao, hivi kwamba akampa dada ya mke wake mwenyewe, dada ya malkia Tapenesi,* ili amwoe. 20 Baada ya muda dada ya Tapenesi akamzalia mwana, Genubathi, na Tapenesi alimlelea* katika nyumba ya Farao; Genubathi aliendelea kukaa katika nyumba ya Farao miongoni mwa wana wa Farao.

21 Hadadi akasikia akiwa Misri kwamba Daudi alikuwa amekufa na kuzikwa pamoja na mababu zake+ na kwamba Yoabu mkuu wa jeshi alikuwa amekufa.+ Basi Hadadi akamwambia Farao: “Niruhusu niende zangu, niende katika ardhi yangu mwenyewe.” 22 Lakini Farao akamuuliza: “Ni nini ulichokosa kwangu hivi kwamba unataka kwenda katika ardhi yako mwenyewe?” Hadadi akamjibu: “Sijakosa chochote, lakini tafadhali niruhusu niende zangu.”

23 Mungu akatokeza pia mtu mwingine wa kumpinga Sulemani,+ yaani, Rezoni mwana wa Eliada, aliyekuwa amemkimbia bwana wake, Hadadezeri+ mfalme wa Soba. 24 Alijikusanyia wanaume akawa kiongozi wa kundi la wavamizi wakati Daudi alipowashinda.*+ Basi wakaenda Damasko,+ wakakaa huko na kuanza kutawala huko Damasko. 25 Naye akawa mpinzani wa Waisraeli siku zote za Sulemani, kuongezea madhara yaliyosababishwa na Hadadi, naye aliwachukia sana Waisraeli alipokuwa akitawala Siria.

26 Pia kulikuwa na Yeroboamu+ mwana wa Nebati, Mwefraimu kutoka Sereda, mtumishi wa Sulemani,+ na mama yake aliyekuwa mjane aliitwa Serua. Yeye pia alianza kumwasi* mfalme.+ 27 Hii ndiyo sababu iliyomfanya amwasi mfalme: Sulemani alikuwa amejenga Kilima*+ na kuziba mwanya katika ukuta wa Jiji la Daudi baba yake.+ 28 Sasa huyu Yeroboamu alikuwa mwanamume mwenye uwezo mkubwa. Sulemani alipoona kwamba kijana huyo alikuwa mfanyakazi mwenye bidii, alimweka kuwa msimamizi+ wa utumishi wote wa lazima wa nyumba ya Yosefu. 29 Wakati huo Yeroboamu alitoka Yerusalemu, na nabii Ahiya,+ Mshilo, akamkuta njiani. Ahiya alikuwa amevaa nguo mpya, na wote wawili walikuwa peke yao shambani. 30 Ahiya akashika nguo mpya aliyokuwa amevaa na kuirarua vipande 12. 31 Kisha akamwambia Yeroboamu:

“Jichukulie vipande kumi, kwa maana Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Tazama, ninaurarua ufalme kutoka mikononi mwa Sulemani, nami nitakupa makabila kumi.+ 32 Lakini atabaki na kabila moja+ kwa ajili ya mtumishi wangu Daudi+ na kwa ajili ya Yerusalemu, jiji ambalo nimechagua miongoni mwa makabila yote ya Israeli.+ 33 Nitafanya hivyo kwa sababu wameniacha,+ nao wanamwinamia Ashtorethi, mungu wa kike wa Wasidoni, na Kemoshi, mungu wa Moabu, na Milkomu, mungu wa Waamoni, nao hawajatembea katika njia zangu kwa kufanya yaliyo sawa machoni pangu na kushika maagizo yangu na sheria zangu* kama Daudi baba yake alivyofanya. 34 Lakini sitauchukua ufalme wote kutoka mikononi mwake, nami nitamwacha aendelee kuwa mkuu sikuzote za maisha yake, kwa ajili ya Daudi mtumishi wangu niliyemchagua,+ kwa sababu alitii amri zangu na sheria zangu. 35 Lakini nitauchukua ufalme kutoka mikononi mwa mwana wake na kukupa wewe, yaani, makabila kumi.+ 36 Nitampa mwana wake kabila moja, ili sikuzote Daudi mtumishi wangu awe na taa mbele zangu Yerusalemu,+ jiji ambalo nimejichagulia liwe mahali pa kuweka jina langu. 37 Nitakuchukua wewe, nawe utatawala kila kitu unachotamani,* nawe utakuwa mfalme wa Israeli. 38 Na ikiwa utatii mambo yote ninayokuamuru na kutembea katika njia zangu na kufanya yaliyo sawa machoni pangu kwa kutii sheria zangu na amri zangu, kama Daudi mtumishi wangu alivyofanya,+ nitakuwa pia pamoja nawe. Nitakujengea nyumba inayodumu, kama nilivyomjengea Daudi,+ nami nitakupa Israeli. 39 Nami nitauaibisha uzao wa Daudi kwa sababu ya jambo hili,+ lakini sitafanya hivyo sikuzote.’”+

40 Basi Sulemani akajaribu kumuua Yeroboamu, lakini Yeroboamu akakimbilia Misri, kwa Mfalme Shishaki+ wa Misri,+ akaendelea kukaa Misri mpaka Sulemani alipokufa.

41 Na mambo mengine katika historia ya Sulemani, mambo yote aliyofanya na hekima yake, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya Sulemani?+ 42 Sulemani alitawala nchi yote ya Israeli kwa miaka 40 akiwa Yerusalemu. 43 Kisha Sulemani akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi baba yake; na Rehoboamu+ mwanawe akawa mfalme baada yake.

12 Rehoboamu alienda Shekemu, kwa maana Waisraeli wote walikuwa wamekuja Shekemu+ kumfanya kuwa mfalme.+ 2 Mara tu Yeroboamu mwana wa Nebati aliposikia habari hizo (bado alikuwa akiishi Misri kwa sababu alikuwa amemkimbia Mfalme Sulemani),+ 3 wakawatuma watu waende kumwita. Kisha Yeroboamu na Waisraeli wote wakaja kwa Rehoboamu na kumwambia hivi: 4 “Baba yako aliifanya nira yetu kuwa nzito.+ Lakini ukiufanya utumishi mzito wa baba yako kuwa mwepesi zaidi na kupunguza nira nzito* aliyotutwika, tutakutumikia.”

5 Ndipo akawaambia: “Nendeni, kisha mrudi baada ya siku tatu.” Basi watu wakaenda zao.+ 6 Kisha Mfalme Rehoboamu akashauriana na wanaume wazee waliomtumikia Sulemani baba yake alipokuwa hai, akawauliza: “Mnanishauri niwape jibu gani watu hawa?” 7 Wakamjibu: “Leo ukiwa mtumishi wa watu hawa na kukubali ombi lao na kuwapa jibu linalofaa, watakuwa watumishi wako sikuzote.”

8 Hata hivyo, alikataa ushauri aliopewa na wanaume wazee, akashauriana na vijana wa rika lake na ambao sasa walikuwa watumishi wake.+ 9 Aliwauliza: “Mnashauri tuwape jibu gani watu hawa ambao wameniambia, ‘Ifanye nira ambayo baba yako alitutwika iwe nyepesi zaidi’?” 10 Vijana hao wa rika lake wakamwambia: “Hivi ndivyo unavyopaswa kuwaambia watu hao waliokwambia, ‘Baba yako aliifanya nira yetu kuwa nzito, lakini wewe unapaswa kuifanya kuwa nyepesi zaidi kwa ajili yetu’; hivi ndivyo unavyopaswa kuwaambia, ‘Kidole changu kidogo kitakuwa kinene kuliko kiuno cha baba yangu. 11 Baba yangu aliwatwika nira nzito, lakini mimi nitazidisha uzito wa nira yenu. Baba yangu aliwaadhibu kwa mijeledi, lakini mimi nitawaadhibu kwa mijeledi yenye miiba.’”

12 Yeroboamu na watu wote wakaja kwa Rehoboamu siku ya tatu, kama mfalme alivyokuwa amesema: “Rudini kwangu siku ya tatu.”+ 13 Lakini mfalme akawajibu watu kwa ukali, akaukataa ushauri aliopewa na wanaume wazee. 14 Akawajibu kama alivyoshauriwa na vijana wa rika lake, na kusema: “Baba yangu aliifanya nira yenu kuwa nzito, lakini mimi nitazidisha uzito wa nira yenu. Baba yangu aliwaadhibu kwa mijeledi, lakini mimi nitawaadhibu kwa mijeledi yenye miiba.” 15 Basi mfalme hakuwasikiliza watu, kwa sababu Yehova ndiye aliyesababisha badiliko hilo la mambo,+ ili atimize neno ambalo Yehova alimwambia Yeroboamu mwana wa Nebati kupitia Ahiya+ Mshilo.

16 Waisraeli wote walipoona kwamba mfalme amekataa kuwasikiliza, wakamwambia hivi mfalme: “Tuna ushirika gani na Daudi? Hatuna urithi wowote katika mwana wa Yese. Nendeni kwa miungu yenu, enyi Waisraeli! Sasa itunze nyumba yako mwenyewe, Ee Daudi!” Ndipo Waisraeli wakarudi katika nyumba zao.*+ 17 Lakini Rehoboamu akaendelea kuwatawala Waisraeli walioishi katika majiji ya Yuda.+

18 Kisha Mfalme Rehoboamu akamtuma Adoramu,+ aliyekuwa msimamizi wa watu waliofanya kazi ya kulazimishwa, lakini Waisraeli wote wakamuua kwa kumpiga mawe. Mfalme Rehoboamu akafaulu kupanda gari lake na kukimbilia Yerusalemu.+ 19 Na tangu siku hiyo Waisraeli wamekuwa wakiiasi+ nyumba ya Daudi.

20 Mara tu Waisraeli wote waliposikia kwamba Yeroboamu amerudi, wakamwita mbele ya kusanyiko, nao wakamweka kuwa mfalme wa Waisraeli wote.+ Hakuna yeyote aliyeifuata nyumba ya Daudi isipokuwa kabila la Yuda.+

21 Rehoboamu alipofika Yerusalemu, mara moja aliikusanya nyumba yote ya Yuda na kabila la Benjamini, mashujaa 180,000 waliozoezwa,* ili wapigane na nyumba ya Israeli na kuurudisha ufalme kwa Rehoboamu mwana wa Sulemani.+ 22 Kisha neno hili la Mungu wa kweli likamjia Shemaya+ mtu wa Mungu wa kweli: 23 “Mwambie Rehoboamu mwana wa Sulemani mfalme wa Yuda na nyumba yote ya Yuda na Benjamini na watu wengine, 24 ‘Hivi ndivyo Yehova anavyosema: “Msipande kwenda kupigana na ndugu zenu Waisraeli. Kila mmoja wenu anapaswa kurudi nyumbani kwake, kwa maana nimesababisha mambo haya yatukie.”’”+ Basi wakalitii neno la Yehova na kurudi nyumbani, kama Yehova alivyowaambia.

25 Kisha Yeroboamu akalijenga* jiji la Shekemu+ katika eneo lenye milima la Efraimu na kuishi humo. Kutoka huko, akaenda kulijenga* jiji la Penueli.+ 26 Yeroboamu akasema moyoni mwake: “Sasa ufalme utarudi katika nyumba ya Daudi.+ 27 Watu hawa wakiendelea kupanda kwenda kutoa dhabihu katika nyumba ya Yehova huko Yerusalemu,+ mioyo ya watu hawa itamrudia pia bwana wao, Mfalme Rehoboamu wa Yuda. Naam, wataniua na kumrudia Mfalme Rehoboamu wa Yuda.” 28 Baada ya kushauriana, mfalme akatengeneza ndama wawili wa dhahabu+ na kuwaambia watu: “Inachosha sana kwenu kupanda kwenda Yerusalemu. Ndiye huyu hapa Mungu wenu, enyi Waisraeli, aliyewatoa nchini Misri.”+ 29 Kisha akamweka ndama mmoja kule Betheli,+ na mwingine akamweka kule Dani.+ 30 Na jambo hilo likawafanya watende dhambi,+ watu wakaenda mpaka Dani kuabudu ndama aliyekuwa huko.

31 Naye akajenga nyumba za ibada mahali pa juu na kuchagua makuhani kutoka miongoni mwa watu wa kawaida, ambao hawakuwa Walawi.+ 32 Pia, Yeroboamu akaanzisha sherehe katika mwezi wa nane, siku ya 15 ya mwezi huo, kama ile sherehe iliyokuwa ikifanywa kule Yuda.+ Kwenye madhabahu aliyojenga kule Betheli,+ alitoa dhabihu kwa wale ndama aliokuwa ametengeneza, na huko Betheli akaweka makuhani wahudumu mahali pa juu alipokuwa amejenga. 33 Katika siku ya 15 ya mwezi wa nane, mwezi aliojichagulia, akaanza kutoa dhabihu kwenye madhabahu aliyokuwa amejenga huko Betheli; akaanzisha sherehe kwa ajili ya Waisraeli, naye akapanda juu ya madhabahu ili kutoa dhabihu na kufukiza moshi wa dhabihu.

13 Kwa neno la Yehova, mtu fulani wa Mungu+ alikuja Betheli kutoka Yuda wakati Yeroboamu alipokuwa amesimama karibu na madhabahu+ ili kufukiza moshi wa dhabihu. 2 Kisha kwa neno la Yehova akapaza sauti dhidi ya madhabahu hiyo na kusema: “Ee madhabahu, madhabahu! Hivi ndivyo Yehova anavyosema, ‘Tazama! Mwana anayeitwa Yosia,+ atazaliwa katika nyumba ya Daudi! Na juu yako atawatoa dhabihu makuhani wa mahali pa juu, wanaofukiza moshi wa dhabihu juu yako, naye atateketeza mifupa ya wanadamu juu yako.’”+ 3 Akatoa ishara* siku hiyo, akisema: “Hii ndiyo ishara* ambayo Yehova ametangaza: Tazama! Madhabahu itapasuka, na majivu* yaliyo juu yake yatamwagika.”

4 Mara tu mfalme aliposikia neno ambalo mtu wa Mungu wa kweli alikuwa amesema dhidi ya madhabahu huko Betheli, Yeroboamu akanyoosha mkono wake kutoka kwenye madhabahu na kusema: “Mkamateni!”+ Mara moja mkono aliokuwa amemnyooshea ukakauka,* naye hakuweza kuurudisha nyuma.+ 5 Kisha madhabahu ikapasuka na majivu yakamwagika kutoka kwenye madhabahu kulingana na ile ishara* ambayo mtu wa Mungu wa kweli alitoa kwa neno la Yehova.

6 Sasa mfalme akamwambia mtu wa Mungu wa kweli: “Tafadhali, niombee kibali kutoka kwa* Yehova Mungu wako, na usali kwa ajili yangu ili nirudishiwe mkono wangu.”+ Ndipo yule mtu wa Mungu wa kweli akaomba kibali kutoka kwa Yehova, na mkono wa mfalme ukarudi kama ulivyokuwa mwanzoni. 7 Kisha mfalme akamwambia mtu wa Mungu wa kweli: “Twende nyumbani ukale chakula, nami nitakupa zawadi.” 8 Lakini mtu wa Mungu wa kweli akamwambia mfalme: “Hata ukinipa nusu ya nyumba yako, siwezi kwenda pamoja nawe na kula mkate au kunywa maji mahali hapa. 9 Kwa maana hivi ndivyo nilivyoamriwa kwa neno la Yehova: ‘Hupaswi kula mkate wala kunywa maji, nawe hupaswi kurudi kwa kutumia njia uliyopitia ulipokuja hapa.’” 10 Basi akaondoka kupitia njia nyingine, naye hakurudi kwa kutumia njia aliyopitia alipokuja Betheli.

11 Kulikuwa na nabii fulani mzee aliyekaa Betheli, wanawe wakaja nyumbani na kumsimulia mambo yote ambayo mtu wa Mungu wa kweli alikuwa amefanya siku hiyo kule Betheli na maneno aliyomwambia mfalme. Baada ya kumsimulia baba yao mambo hayo, 12 baba yao akawauliza: “Alipitia njia gani?” Kwa hiyo wanawe wakamwonyesha njia aliyopitia mtu huyo wa Mungu wa kweli aliyetoka Yuda. 13 Sasa akawaambia wanawe: “Niwekeeni matandiko juu ya punda.” Basi wakamwekea matandiko juu ya punda, naye akapanda juu yake.

14 Akamfuata mtu wa Mungu wa kweli na kumkuta ameketi chini ya mti mkubwa. Kisha akamuuliza: “Je, wewe ndiye yule mtu wa Mungu wa kweli aliyetoka Yuda?”+ Akajibu: “Ni mimi.” 15 Akamwambia: “Twende nyumbani ukale mkate.” 16 Lakini akasema: “Siwezi kurudi pamoja nawe wala kukubali mwaliko wako, nami siwezi kula mkate wala kunywa maji pamoja nawe mahali hapa. 17 Kwa maana niliambiwa kwa neno la Yehova, ‘Hupaswi kula mkate wala kunywa maji huko. Hupaswi kurudi kupitia njia uliyotumia kuja.’” 18 Ndipo akamwambia: “Mimi pia ni nabii kama wewe, na malaika aliniambia hivi kwa neno la Yehova: ‘Mwambie arudi pamoja nawe nyumbani kwako ili ale mkate na kunywa maji.’” (Alimdanganya.) 19 Basi akarudi pamoja naye ili ale mkate na kunywa maji nyumbani kwake.

20 Walipokuwa wameketi mezani, neno la Yehova likamjia nabii aliyekuwa amemrudisha, 21 naye akamwambia kwa sauti yule mtu wa Mungu wa kweli aliyetoka Yuda: “Yehova anasema hivi: ‘Kwa sababu uliasi agizo la Yehova, nawe hukushika amri ambayo Yehova Mungu wako alikupa, 22 lakini ulirudi kula mkate na kunywa maji mahali ambapo uliambiwa, “Usile mkate wala kunywa maji,” maiti yako haitazikwa katika makaburi ya mababu zako.’”+

23 Baada ya mtu wa Mungu wa kweli kula mkate na kunywa maji, nabii mzee akaweka matandiko juu ya punda kwa ajili ya nabii aliyekuwa amemrudisha. 24 Kisha akaenda zake, lakini simba akakutana naye barabarani na kumuua.+ Maiti yake ikatupwa barabarani, na punda akasimama kando yake; simba pia alikuwa amesimama kando ya maiti hiyo. 25 Watu waliokuwa wakipita hapo waliona maiti hiyo ikiwa imetupwa barabarani na simba akiwa amesimama kando yake. Wakaenda na kusimulia habari hizo katika jiji ambamo yule nabii mzee alikuwa akiishi.

26 Nabii huyo aliyekuwa amemrudisha njiani aliposikia habari hizo, mara moja akasema: “Ni yule mtu wa Mungu wa kweli aliyeasi agizo la Yehova;+ kwa hiyo Yehova alimkabidhi kwa simba, amrarue na kumuua, kulingana na neno la Yehova alilokuwa amemwambia.”+ 27 Kisha akawaambia hivi wanawe: “Niwekeeni matandiko juu ya punda.” Basi wakaweka matandiko juu yake. 28 Halafu akaenda zake na kuikuta ile maiti imetupwa barabarani, punda na simba wakiwa wamesimama kando ya maiti hiyo. Simba hakuwa ameila maiti, wala hakuwa amemrarua punda. 29 Nabii huyo mzee akaibeba maiti ya mtu wa Mungu wa kweli na kuiweka juu ya punda, akairudisha katika jiji lake mwenyewe ili kumwombolezea na kumzika. 30 Basi akailaza maiti hiyo katika kaburi lake mwenyewe, nao wakaendelea kumlilia kwa sauti wakisema: “Ole wako, ndugu yangu!” 31 Baada ya kumzika, akawaambia wanawe: “Nitakapokufa, nizikeni mahali ambapo mtu wa Mungu wa kweli amezikwa. Ilazeni mifupa yangu kando ya mifupa yake.+ 32 Neno la Yehova alilokuwa ametangaza dhidi ya madhabahu iliyoko Betheli na dhidi ya nyumba zote za ibada zilizo mahali pa juu+ katika majiji ya Samaria hakika litatimia.”+

33 Hata baada ya mambo hayo kutendeka, Yeroboamu hakuacha njia yake mbaya, lakini aliendelea kuchagua makuhani kutoka miongoni mwa watu wa kawaida ili wahudumu mahali pa juu.+ Alimweka kuwa kuhani* mtu yeyote aliyetaka kuwa kuhani, akisema: “Na awe mmoja wa makuhani wa mahali pa juu.”+ 34 Dhambi hiyo ya nyumba ya Yeroboamu+ ilisababisha waharibiwe na kuangamizwa kutoka duniani.+

14 Wakati huo Abiya mwana wa Yeroboamu akawa mgonjwa. 2 Kwa hiyo Yeroboamu akamwambia mke wake: “Tafadhali, inuka, badili sura yako ili watu wasitambue kwamba wewe ni mke wa Yeroboamu, halafu uende Shilo. Tazama! Nabii Ahiya yuko huko. Yeye ndiye aliyesema kwamba mimi nitakuwa mfalme wa watu hawa.+ 3 Chukua mikate kumi, keki zilizonyunyiziwa kitu, na chupa ya asali, uende kwake. Kisha atakwambia kitakachompata mvulana huyu.”

4 Mke wa Yeroboamu akafanya mambo aliyoambiwa na Yeroboamu. Akainuka na kwenda Shilo,+ akafika katika nyumba ya Ahiya. Ahiya alikodoa macho yake mbele, lakini hakuweza kuona kwa sababu ya umri wake.

5 Hata hivyo, Yehova alikuwa amemwambia Ahiya: “Tazama, mke wa Yeroboamu anakuja kutafuta habari kuhusu mwanawe, kwa sababu ni mgonjwa. Nitakwambia mambo utakayomwambia.* Atakapofika ataficha sura yake ili asijulikane.”

6 Mara tu Ahiya aliposikia sauti ya miguu ya mwanamke huyo alipokuwa akija mlangoni, akasema: “Ingia ndani, mke wa Yeroboamu. Kwa nini unaficha sura yako usijulikane? Nimeagizwa nikupe ujumbe mkali. 7 Nenda, ukamwambie Yeroboamu, ‘Hivi ndivyo anavyosema Yehova Mungu wa Israeli: “Nilikuinua kutoka miongoni mwa watu wako na kukufanya kuwa kiongozi wa watu wangu Waisraeli.+ 8 Kisha nikaurarua ufalme kutoka katika nyumba ya Daudi na kukupa wewe.+ Lakini hujawa kama mtumishi wangu Daudi, ambaye alishika amri zangu na kunifuata kwa moyo wake wote, akitenda tu yaliyokuwa sawa machoni pangu.+ 9 Lakini umetenda mambo mabaya zaidi kuliko wote waliokutangulia, nawe ulijitengenezea mungu mwingine na sanamu za chuma* ili kunikasirisha,+ mimi ndiye uliyenigeuzia mgongo.+ 10 Kwa sababu hiyo ninailetea msiba nyumba ya Yeroboamu, nami nitamwangamiza kila mwanamume* wa Yeroboamu, kutia ndani wasio na uwezo na walio dhaifu katika Israeli, nami nitaifagia kabisa nyumba ya Yeroboamu,+ kama mtu anavyoondoa kabisa mavi mpaka yote yanapokwisha! 11 Mtu yeyote wa Yeroboamu atakayefia jijini, ataliwa na mbwa; na yeyote atakayefia shambani, ataliwa na ndege wa angani, kwa sababu Yehova amesema hayo.”’

12 “Sasa inuka; nenda nyumbani kwako. Utakapotia mguu wako jijini, mtoto huyo atakufa. 13 Waisraeli wote watamwombolezea na kumzika, kwa maana ni yeye peke yake katika familia ya Yeroboamu atakayezikwa kaburini, kwa sababu ni yeye tu katika nyumba ya Yeroboamu ambaye Yehova Mungu wa Israeli amepata jambo fulani jema ndani yake. 14 Yehova atajiinulia mfalme wa Israeli atakayeiangamiza nyumba ya Yeroboamu+ kuanzia siku hiyo na kuendelea, naam, hata sasa. 15 Yehova atawapiga Waisraeli kama tete linaloyumba-yumba ndani ya maji, naye atawang’oa Waisraeli kutoka katika nchi hii nzuri aliyowapa mababu zao+ na kuwatawanya ng’ambo ya Mto Efrati,+ kwa sababu walimkasirisha Yehova kwa kutengeneza miti mitakatifu.*+ 16 Naye atawaacha Waisraeli kwa sababu ya dhambi ambazo Yeroboamu alitenda na kusababisha Waisraeli kuzitenda.”+

17 Basi mke wa Yeroboamu akainuka na kwenda zake, akafika Tirsa. Alipokaribia kizingiti cha mlango, mvulana huyo akafa. 18 Kwa hiyo wakamzika, na Waisraeli wote wakamwombolezea, kama Yehova alivyokuwa amesema kupitia nabii Ahiya, mtumishi wake.

19 Na mambo mengine katika historia ya Yeroboamu, jinsi alivyopigana vita+ na jinsi alivyotawala, yameandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli. 20 Yeroboamu alitawala kwa miaka 22, kisha akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake;+ na Nadabu mwanawe akawa mfalme baada yake.+

21 Wakati huo, Rehoboamu mwana wa Sulemani alikuwa mfalme wa Yuda. Rehoboamu alikuwa na umri wa miaka 41 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 17 huko Yerusalemu, jiji ambalo Yehova alichagua+ miongoni mwa makabila yote ya Israeli ili kuweka jina lake humo.+ Mama ya Rehoboamu aliitwa Naama, naye alikuwa Mwamoni.+ 22 Na watu wa Yuda walikuwa wakitenda maovu machoni pa Yehova,+ na kwa dhambi zao walimkasirisha kuliko walivyofanya mababu zao.+ 23 Pia waliendelea kujijengea mahali pa juu, nguzo takatifu, na miti mitakatifu*+ juu ya kila kilima kirefu+ na chini ya kila mti wenye majani mengi.+ 24 Kulikuwa pia na wanaume makahaba wa hekaluni katika nchi.+ Watu walitenda mambo yote yenye kuchukiza yaliyofanywa na mataifa ambayo Yehova alikuwa ameyafukuza kutoka mbele ya Waisraeli.

25 Katika mwaka wa tano wa Mfalme Rehoboamu, Mfalme Shishaki+ wa Misri alishambulia Yerusalemu.+ 26 Akachukua hazina za nyumba ya Yehova na hazina za nyumba ya mfalme.*+ Alichukua kila kitu, kutia ndani ngao zote za dhahabu ambazo Sulemani alikuwa ametengeneza.+ 27 Basi Mfalme Rehoboamu akatengeneza ngao za shaba zichukue mahali pa ngao hizo, akaziweka chini ya ulinzi wa mkuu wa walinzi,* aliyelinda mlango wa nyumba ya mfalme. 28 Wakati wowote ambapo mfalme alikuja katika nyumba ya Yehova, walinzi walizichukua, kisha walizirudisha katika chumba cha walinzi.

29 Na mambo mengine katika historia ya Rehoboamu, mambo yote aliyofanya, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda?+ 30 Kulikuwa na vita daima kati ya Rehoboamu na Yeroboamu.+ 31 Kisha Rehoboamu akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi.+ Mama yake aliitwa Naama, naye alikuwa Mwamoni.+ Na Abiyamu* mwana wake+ akawa mfalme baada yake.

15 Katika mwaka wa 18 wa utawala wa Mfalme Yeroboamu+ mwana wa Nebati, Abiyamu akawa mfalme wa Yuda.+ 2 Alitawala kwa miaka mitatu huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Maaka,+ mjukuu wa Abishalomu. 3 Aliendelea kutembea katika dhambi zote ambazo baba yake alitenda kabla yake, na moyo wake haukuwa kamili kwa* Yehova Mungu wake kama moyo wa Daudi babu yake. 4 Hata hivyo, kwa sababu ya Daudi,+ Yehova Mungu wake alimpa taa huko Yerusalemu+ kwa kumwinua mwana wake atawale baada yake na kufanya jiji la Yerusalemu lidumu. 5 Kwa maana Daudi alitenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova, naye hakugeuka na kuacha jambo lolote ambalo Yeye alikuwa amemwamuru sikuzote za maisha yake, isipokuwa kuhusiana na kisa cha Uria, Mhiti.+ 6 Na kulikuwa na vita kati ya Rehoboamu na Yeroboamu sikuzote za maisha yake.+

7 Na mambo mengine katika historia ya Abiyamu, mambo yote aliyofanya, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda?+ Kulikuwa pia na vita kati ya Abiyamu na Yeroboamu.+ 8 Kisha Abiyamu akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi; na Asa mwanawe+ akawa mfalme baada yake.+

9 Katika mwaka wa 20 wa Mfalme Yeroboamu wa Israeli, Asa alianza kutawala Yuda. 10 Alitawala Yerusalemu kwa miaka 41. Nyanya yake aliitwa Maaka,+ mjukuu wa Abishalomu. 11 Asa alitenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova,+ kama Daudi babu yake. 12 Aliwafukuza wanaume makahaba wa hekaluni kutoka nchini+ na kuondoa sanamu zote zenye kuchukiza* ambazo mababu zake walikuwa wametengeneza.+ 13 Hata alimwondoa Maaka+ nyanya yake kutoka katika cheo chake cha mama malkia, kwa sababu alikuwa ametengeneza sanamu chafu sana* kwa ajili ya ibada ya mti mtakatifu.* Asa akaikatakata sanamu hiyo chafu sana+ na kuiteketeza katika Bonde la Kidroni.+ 14 Lakini mahali pa juu hapakuondolewa.+ Hata hivyo, moyo wa Asa ulikuwa kamili kwa* Yehova maisha yake yote.* 15 Naye alileta katika nyumba ya Yehova vitu ambavyo yeye na baba yake walikuwa wamevifanya kuwa vitakatifu—fedha, dhahabu, na vyombo mbalimbali.+

16 Kulikuwa na vita daima kati ya Asa na Baasha+ mfalme wa Israeli. 17 Basi Mfalme Baasha wa Israeli alikuja kushambulia Yuda, akaanza kujenga* Rama+ ili kumzuia mtu yeyote asitoke wala kuingia kwa* Mfalme Asa wa Yuda.+ 18 Ndipo Asa akachukua fedha yote na dhahabu iliyokuwa imebaki katika hazina za nyumba ya Yehova na hazina za nyumba ya* mfalme na kuwapa watumishi wake. Kisha Mfalme Asa akawatuma kwa Ben-hadadi mwana wa Tabrimoni mwana wa Hezioni, mfalme wa Siria,+ aliyekuwa akiishi Damasko, akamwambia: 19 “Kuna mkataba* kati yangu na wewe na kati ya baba yangu na baba yako. Ninakutumia zawadi ya fedha na dhahabu. Njoo, vunja mkataba wako* na Mfalme Baasha wa Israeli, ili aondoke kwangu.” 20 Ben-hadadi akamsikiliza Mfalme Asa, akawatuma wakuu wa majeshi yake kushambulia majiji ya Israeli, wakashinda Iyoni,+ Dani,+ Abel-beth-maaka, eneo lote la Kinerethi, na nchi yote ya Naftali. 21 Baasha aliposikia habari hizo, mara moja akaacha kujenga* Rama, akaendelea kuishi Tirsa.+ 22 Kisha Mfalme Asa akawaita watu wote wa Yuda—hakuna aliyeachwa—nao wakabeba mawe na mbao zilizokuwa zikitumiwa na Baasha kujenga Rama, Mfalme Asa akazitumia kujenga* Geba+ kule Benjamini, na pia Mispa.+

23 Na mambo mengine katika historia ya Asa, ukuu wake wote na mambo yote aliyofanya na majiji aliyojenga,* je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda? Lakini alipozeeka alishikwa na ugonjwa miguuni.+ 24 Kisha Asa akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi babu yake; na Yehoshafati+ mwanawe akawa mfalme baada yake.

25 Nadabu+ mwana wa Yeroboamu akawa mfalme wa Israeli katika mwaka wa pili wa Mfalme Asa wa Yuda, naye alitawala Israeli kwa miaka miwili. 26 Aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova na kufuata njia ya baba yake+ na dhambi yake aliyosababisha Waisraeli kutenda.+ 27 Baasha mwana wa Ahiya wa nyumba ya Isakari akapanga njama dhidi yake, na Baasha akamuua kule Gibethoni,+ jiji la Wafilisti, wakati Nadabu na Waisraeli wote walipokuwa wakilizingira Gibethoni. 28 Kwa hiyo Baasha akamuua katika mwaka wa tatu wa Mfalme Asa wa Yuda, akawa mfalme baada yake. 29 Mara tu alipokuwa mfalme, aliiangamiza nyumba yote ya Yeroboamu. Hakumwacha mtu yeyote wa Yeroboamu akipumua; aliagiza waangamizwe kama Yehova alivyokuwa amesema kupitia Ahiya, mtumishi wake kutoka Shilo.+ 30 Alifanya hivyo kwa sababu ya dhambi ambazo Yeroboamu alikuwa ametenda na kusababisha Waisraeli wazitende na kwa sababu alikuwa amemkasirisha sana Yehova Mungu wa Israeli. 31 Na mambo mengine katika historia ya Nadabu, mambo yote aliyofanya, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli? 32 Na kulikuwa na vita daima kati ya Asa na Mfalme Baasha wa Israeli.+

33 Katika mwaka wa tatu wa Mfalme Asa wa Yuda, Baasha mwana wa Ahiya akawa mfalme wa Waisraeli wote kule Tirsa, alitawala kwa miaka 24.+ 34 Lakini aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova,+ akafuata njia ya Yeroboamu na dhambi yake ambayo alisababisha Waisraeli kutenda.+

16 Kisha neno hili la Yehova dhidi ya Baasha likamjia Yehu+ mwana wa Hanani:+ 2 “Nilikuinua kutoka mavumbini na kukufanya kuwa kiongozi wa watu wangu Waisraeli,+ lakini uliendelea kutembea katika njia ya Yeroboamu na kusababisha watu wangu Waisraeli watende dhambi hivi kwamba walinikasirisha kwa dhambi zao.+ 3 Kwa hiyo ninamfagilia mbali Baasha na nyumba yake, nami nitaifanya nyumba yake kuwa kama nyumba ya Yeroboamu+ mwana wa Nebati. 4 Mtu yeyote wa nyumba ya Baasha anayefia jijini ataliwa na mbwa; na mtu yeyote wa nyumba yake anayefia shambani ataliwa na ndege wa angani.”

5 Na mambo mengine katika historia ya Baasha, mambo aliyofanya na ukuu wake, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli? 6 Kisha Baasha akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake kule Tirsa;+ na Ela mwana wake akawa mfalme baada yake. 7 Tena, neno la Yehova dhidi ya Baasha na nyumba yake lilikuja kupitia nabii Yehu mwana wa Hanani, kwa sababu ya uovu wote aliotenda machoni pa Yehova na kumkasirisha kwa kazi za mikono yake, akawa kama nyumba ya Yeroboamu, na pia kwa sababu alimuua Nadabu.*+

8 Katika mwaka wa 26 wa Mfalme Asa wa Yuda, Ela mwana wa Baasha akawa mfalme wa Israeli kule Tirsa, naye alitawala kwa miaka miwili. 9 Zimri mtumishi wake, mkuu wa nusu ya kikosi chake cha magari ya vita, alipanga njama dhidi yake alipokuwa Tirsa akinywa na kulewa nyumbani kwa Arsa, msimamizi wa nyumba yake kule Tirsa. 10 Zimri akaingia, akampiga+ na kumuua katika mwaka wa 27 wa Mfalme Asa wa Yuda, naye akawa mfalme baada yake. 11 Alipokuwa mfalme, mara tu alipoketi kwenye kiti chake cha ufalme, aliiangamiza nyumba yote ya Baasha. Hakumwacha mwanamume yeyote,* iwe ni mtu wake wa ukoo* au ni rafiki yake. 12 Basi Zimri akaiangamiza nyumba yote ya Baasha, kama Yehova alivyokuwa amesema dhidi ya Baasha kupitia nabii Yehu.+ 13 Alifanya hivyo kwa sababu ya dhambi zote ambazo Baasha na mwanawe Ela walikuwa wametenda na dhambi ambazo walisababisha Waisraeli kutenda na kumkasirisha Yehova Mungu wa Israeli kwa sanamu zao za ubatili.+ 14 Na mambo mengine katika historia ya Ela, mambo yote aliyofanya, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli?

15 Katika mwaka wa 27 wa Mfalme Asa wa Yuda, Zimri akawa mfalme kwa siku saba kule Tirsa wanajeshi walipokuwa wamepiga kambi dhidi ya Gibethoni,+ jiji la Wafilisti. 16 Baada ya muda wanajeshi waliokuwa wamepiga kambi wakasikia hivi: “Zimri amepanga njama na pia amemuua mfalme.” Basi siku hiyo huko kambini Waisraeli wote wakamweka Omri,+ mkuu wa jeshi, kuwa mfalme wa Israeli. 17 Omri na Waisraeli wote wakapanda kutoka Gibethoni na kulizingira Tirsa. 18 Zimri alipoona kwamba jiji limetekwa, akaingia katika mnara wenye ngome wa nyumba ya mfalme* na kuiteketeza kwa moto akiwa ndani yake, naye akafa.+ 19 Alifanya hivyo kwa sababu ya dhambi zake mwenyewe alizofanya alipotenda maovu machoni pa Yehova kwa kutembea katika njia ya Yeroboamu na kwa sababu ya dhambi aliyosababisha Waisraeli wafanye.+ 20 Na mambo mengine katika historia ya Zimri pamoja na njama yake, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli?

21 Wakati huo ndipo watu wa Israeli walipogawanyika makundi mawili. Kundi moja lilimfuata Tibni mwana wa Ginathi likitaka kumfanya kuwa mfalme, na kundi lingine likamfuata Omri. 22 Lakini watu waliokuwa wakimfuata Omri waliwashinda watu waliokuwa wakimfuata Tibni mwana wa Ginathi. Basi Tibni akafa, na Omri akawa mfalme.

23 Katika mwaka wa 31 wa Mfalme Asa wa Yuda, Omri akawa mfalme wa Israeli, naye akatawala kwa miaka 12. Alitawala Tirsa kwa miaka sita. 24 Alinunua mlima wa Samaria kutoka kwa Shemeri kwa talanta mbili za fedha,* akajenga jiji juu ya mlima huo. Jiji alilojenga aliliita Samaria,*+ jina la Shemeri mmiliki* wa mlima huo. 25 Omri akaendelea kutenda maovu machoni pa Yehova, akatenda maovu kuliko wote waliomtangulia.+ 26 Alitembea katika njia zote za Yeroboamu mwana wa Nebati na katika dhambi aliyokuwa amesababisha Waisraeli wafanye na kumkasirisha Yehova Mungu wa Israeli kwa sanamu zao za ubatili.+ 27 Na mambo mengine katika historia ya Omri, mambo aliyofanya na mambo makuu aliyotekeleza, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli? 28 Kisha Omri akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake huko Samaria; na Ahabu+ mwana wake akawa mfalme baada yake.

29 Ahabu mwana wa Omri akawa mfalme wa Israeli katika mwaka wa 38 wa Mfalme Asa wa Yuda, na Ahabu mwana wa Omri akatawala Israeli kwa miaka 22 huko Samaria.+ 30 Ahabu mwana wa Omri alikuwa mwovu sana machoni pa Yehova kuliko wote waliomtangulia.+ 31 Na kana kwamba lilikuwa jambo dogo kwake kutembea katika dhambi za Yeroboamu+ mwana wa Nebati, hata alimwoa Yezebeli+ binti ya Ethbaali, mfalme wa Wasidoni,+ akaanza kumwabudu Baali+ na kumwinamia. 32 Isitoshe, alisimamisha madhabahu kwa ajili ya Baali katika nyumba ya Baali+ aliyoijenga* kule Samaria. 33 Ahabu pia alitengeneza mti mtakatifu.*+ Ahabu alifanya mambo mengi zaidi yaliyomkasirisha Yehova Mungu wa Israeli kuliko wafalme wote wa Israeli waliomtangulia.

34 Katika siku zake, Hieli kutoka Betheli alijenga upya Yeriko. Alipojenga msingi wake, Abiramu mzaliwa wake wa kwanza alikufa, na alipoweka malango yake, Segubu mwana wake wa mwisho akafa, kama Yehova alivyokuwa amesema kupitia Yoshua mwana wa Nuni.+

17 Sasa Eliya*+ Mtishbi, mkaaji wa Gileadi,+ alimwambia hivi Ahabu: “Kwa hakika kama anavyoishi Yehova Mungu wa Israeli ninayemtumikia,* katika miaka hii hakutakuwa na umande wala mvua isipokuwa kwa neno langu!”+

2 Neno hili la Yehova likamjia: 3 “Ondoka hapa, ugeuke kwenda upande wa mashariki, ujifiche katika Bonde* la Kerithi, upande wa mashariki wa Yordani. 4 Utakunywa maji kutoka katika kijito, nami nitawaamuru kunguru wakuletee chakula huko.”+ 5 Akaenda mara moja na kutenda kulingana na neno la Yehova; alienda kukaa katika Bonde* la Kerithi, upande wa mashariki wa Yordani. 6 Na kunguru walikuwa wakimletea mkate na nyama asubuhi na mkate na nyama jioni, naye alikunywa maji kutoka katika kile kijito.+ 7 Lakini baada ya siku kadhaa, kijito hicho kikakauka+ kwa sababu mvua haikunyesha nchini.

8 Basi neno hili la Yehova likamjia: 9 “Ondoka, nenda Sarefathi ya Sidoni, nawe ukae huko. Tazama! Nitamwamuru mjane fulani huko akupe chakula.”+ 10 Basi akainuka na kwenda Sarefathi. Alipofika kwenye lango la jiji, kulikuwa na mwanamke fulani mjane aliyekuwa akiokota kuni. Basi akamwita mwanamke huyo na kumwambia: “Tafadhali, niletee maji kidogo kwenye kikombe ninywe.”+ 11 Alipokuwa akienda kuyaleta, Eliya akamwita na kumwambia: “Tafadhali, niletee kipande cha mkate.” 12 Ndipo mwanamke huyo akasema: “Kwa hakika kama Yehova Mungu wako anavyoishi, sina mkate, nina konzi moja tu ya unga katika mtungi mkubwa na mafuta kidogo katika mtungi mdogo.+ Sasa ninaokota kuni chache tu, kisha niende nyumbani na kupika chakula kidogo kwa ajili yangu na mwanangu. Baada ya kula chakula hicho, tutakufa.”

13 Kisha Eliya akamwambia: “Usiogope. Nenda nyumbani ufanye kama ulivyosema. Lakini kwanza nitayarishie mkate mdogo wa mviringo kwa unga na mafuta uliyo nayo. Kisha unaweza kutayarisha chochote baadaye kwa ajili yako na mwanao. 14 Kwa maana Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Unga ulio katika huo mtungi mkubwa hautakwisha, na mafuta yaliyo katika huo mtungi mdogo hayatakwisha mpaka siku ambayo Yehova ataleta mvua nchini.’”+ 15 Basi akaenda na kufanya kama Eliya alivyosema; mwanamke huyo pamoja na Eliya na familia ya mwanamke huyo wakawa na chakula kwa siku nyingi.+ 16 Unga uliokuwa katika mtungi huo mkubwa haukwisha, na mafuta yaliyokuwa katika mtungi ule mdogo hayakwisha, kama Yehova alivyokuwa amesema kupitia Eliya.

17 Baada ya mambo hayo, mwana wa mwanamke huyo mwenye nyumba akawa mgonjwa, na hali yake ikawa mbaya sana hivi kwamba akakata pumzi.+ 18 Ndipo mwanamke huyo akamuuliza Eliya: “Nimekukosea nini, ewe mtu wa Mungu wa kweli? Je, umekuja kunikumbusha hatia yangu na kumuua mwanangu?”+ 19 Lakini Eliya akamwambia: “Nipe mwana wako.” Kisha akamchukua kutoka mikononi mwake, akambeba hadi katika chumba cha darini, alimokuwa akikaa, akamlaza kwenye kitanda chake mwenyewe.+ 20 Akamlilia Yehova kwa sauti akisema: “Ee Yehova Mungu wangu,+ je, unamdhuru pia mjane ninayekaa kwake kwa kumuua mwanawe?” 21 Kisha akajinyoosha juu ya mtoto huyo mara tatu na kumlilia Yehova kwa sauti akisema: “Ee Yehova Mungu wangu, tafadhali, acha uhai wa mtoto huyu umrudie.” 22 Yehova akasikiliza ombi la Eliya,+ na uhai wa mtoto huyo ukamrudia, akawa hai tena.+ 23 Eliya akamchukua mtoto huyo, akamleta chini kutoka katika kile chumba cha darini, akampa mama yake; Eliya akasema: “Tazama, mwana wako yuko hai.”+ 24 Ndipo mwanamke huyo akamwambia Eliya: “Sasa ninajua kwamba kwa kweli wewe ni mtu wa Mungu+ na kwamba neno la Yehova kutoka kinywani mwako ni kweli.”

18 Baada ya muda fulani, katika mwaka wa tatu,+ neno la Yehova likamjia Eliya likisema: “Nenda ukamwone Ahabu, nami nitaleta mvua nchini.”+ 2 Basi Eliya akaenda kumwona Ahabu, wakati huo kulikuwa na njaa kali sana+ Samaria.

3 Wakati huo, Ahabu akamwita Obadia, aliyekuwa msimamizi wa nyumba yake. (Obadia alimwogopa sana Yehova, 4 na Yezebeli+ alipokuwa akiwaua manabii wa Yehova, Obadia aliwachukua manabii 100 na kuwaficha katika mapango mawili, manabii 50 katika kila pango, naye alikuwa akiwapa mikate na maji.) 5 Kisha Ahabu akamwambia Obadia: “Pita kotekote nchini kwenye chemchemi zote za maji na mabonde* yote. Huenda tukapata majani ya kutosha ili farasi na nyumbu waendelee kuishi, wanyama wetu wote wasife.” 6 Kwa hiyo wakagawana maeneo ya nchi ambako wangeenda kutafuta nyasi. Ahabu akaenda peke yake upande mmoja, na Obadia akaenda peke yake upande mwingine.

7 Obadia alipokuwa akienda zake, akakutana na Eliya. Mara moja Obadia akamtambua, akaanguka chini kifudifudi na kumuuliza: “Je, ni wewe, bwana wangu Eliya?”+ 8 Akamjibu: “Ni mimi. Nenda ukamwambie bwana wako, ‘Eliya yuko hapa.’” 9 Lakini akasema: “Nimetenda dhambi gani hivi kwamba unanitia mimi mtumishi wako mikononi mwa Ahabu ili aniue? 10 Kwa hakika kama Yehova Mungu wako anavyoishi, hakuna taifa wala ufalme ambamo bwana wangu hakuwatuma watu wakutafute. Waliposema, ‘Hayuko hapa,’ aliagiza ufalme na taifa hilo liape kwamba limeshindwa kukupata.+ 11 Sasa unasema, ‘Nenda ukamwambie bwana wako: “Eliya yuko hapa.”’ 12 Nitakapokuacha, roho ya Yehova itakubeba na kukupeleka+ mahali ambapo sitajua, nami nikimwambia Ahabu naye asikupate, kwa hakika ataniua. Lakini mimi mtumishi wako nimemwogopa Yehova tangu nilipokuwa kijana. 13 Je, bwana wangu hukuambiwa niliyofanya Yezebeli alipokuwa akiwaua manabii wa Yehova, jinsi nilivyowaficha manabii 100 wa Yehova, manabii 50 katika kila pango, na jinsi nilivyokuwa nikiwapa mikate na maji?+ 14 Lakini sasa unasema, ‘Nenda ukamwambie bwana wako: “Eliya yuko hapa.”’ Hakika ataniua.” 15 Hata hivyo, Eliya akamwambia: “Kwa hakika kama anavyoishi Yehova wa majeshi ninayemtumikia,* nitaenda kumwona leo.”

16 Basi Obadia akaenda kukutana na Ahabu na kumwambia habari hizo, kisha Ahabu akaenda kukutana na Eliya.

17 Mara tu Ahabu alipomwona Eliya akamwambia: “Kumbe ni wewe unayeiletea Israeli taabu kubwa!”*

18 Eliya akasema: “Sijailetea Israeli taabu, lakini ni wewe na nyumba ya baba yako mliofanya hivyo kwa kuziacha amri za Yehova na kufuata Mabaali.+ 19 Na sasa nikusanyie Waisraeli wote kwenye Mlima Karmeli,+ pamoja na manabii 450 wa Baali na manabii 400 wa mti mtakatifu,*+ wanaokula kwenye meza ya Yezebeli.” 20 Basi Ahabu akatuma ujumbe kwa Waisraeli wote, akawakusanya pamoja manabii kwenye Mlima Karmeli.

21 Kisha Eliya akawakaribia watu wote na kusema: “Mtaendelea kuyumbayumba kati ya maoni mawili tofauti*+ mpaka wakati gani? Ikiwa Yehova ndiye Mungu wa kweli, mfuateni;+ lakini ikiwa ni Baali, mfuateni!” Hata hivyo, watu hawakumjibu neno lolote. 22 Ndipo Eliya akawaambia watu: “Mimi peke yangu ndiye nabii wa Yehova aliyebaki,+ lakini manabii wa Baali ni 450. 23 Na watupatie ng’ombe dume wachanga wawili, kisha wachague ng’ombe dume mmoja mchanga na kumkata vipandevipande na kuviweka juu ya kuni, lakini wasiwashe moto. Nitamtayarisha ng’ombe dume mchanga wa pili na kumweka juu ya kuni, lakini sitawasha moto. 24 Kisha mtaliita jina la mungu wenu,+ nami nitaliita jina la Yehova. Mungu atakayejibu kwa moto, atathibitisha kwamba yeye ndiye Mungu wa kweli.”+ Ndipo watu wote wakasema: “Jambo unalosema ni jema.”

25 Sasa Eliya akawaambia manabii wa Baali: “Chagueni ng’ombe dume mmoja mchanga na kumtayarisha kwanza, kwa sababu ninyi ni wengi. Kisha mliite jina la mungu wenu, lakini msiwashe moto.” 26 Basi wakamchukua huyo ng’ombe dume mchanga waliyepewa, wakamtayarisha, na kuendelea kuliita jina la Baali kuanzia asubuhi mpaka adhuhuri, wakisema: “Ee Baali, tujibu!” Lakini hapakuwa na sauti yoyote, wala yeyote aliyewajibu.+ Nao wakazidi kurukaruka kuizunguka madhabahu waliyokuwa wametengeneza. 27 Karibu wakati wa adhuhuri Eliya akaanza kuwadhihaki na kusema: “Iteni kwa sauti yenu yote! Je, si yeye ni mungu?+ Labda amezama katika mawazo au ameenda chooni.* Au pengine amelala usingizi na mtu fulani anahitaji kumwamsha!” 28 Walikuwa wakiita kwa sauti yao yote na kujikatakata kwa visu na mikuki, kulingana na desturi yao, mpaka walipotokwa na damu nyingi mwili mzima. 29 Wakati wa adhuhuri ukapita lakini wakaendelea kutenda kiwazimu* mpaka jioni wakati ambapo toleo la nafaka hutolewa, lakini hapakuwa na sauti yoyote wala yeyote aliyejibu; hakuna aliyewasikiliza.+

30 Hatimaye Eliya akawaambia watu wote: “Nikaribieni.” Basi watu wote wakamkaribia. Kisha akairekebisha madhabahu ya Yehova iliyokuwa imebomolewa.+ 31 Halafu Eliya akachukua mawe 12, kulingana na idadi ya makabila ya wana wa Yakobo, ambaye neno la Yehova lilikuwa limemjia likisema: “Jina lako litakuwa Israeli.”+ 32 Akatumia mawe hayo kujenga madhabahu+ katika jina la Yehova. Kisha akachimba mtaro kuzunguka madhabahu hiyo, eneo kubwa ambalo lilitosha kupandwa sea mbili* za mbegu. 33 Kisha akapanga kuni, akamkata yule ng’ombe dume mchanga vipandevipande na kuviweka juu ya hizo kuni.+ Halafu akasema: “Ijazeni maji mitungi mikubwa minne, myamwage juu ya dhabihu ya kuteketezwa na juu ya kuni.” 34 Kisha akasema: “Fanyeni hivyo tena.” Basi wakafanya hivyo tena. Akasema tena: “Fanyeni hivyo mara ya tatu.” Basi wakafanya hivyo mara ya tatu. 35 Maji yakajaa kuizunguka madhabahu, na pia akaujaza mtaro maji.

36 Karibu wakati wa kutoa toleo la nafaka la jioni,+ nabii Eliya akaja mbele na kusema: “Ee Yehova, Mungu wa Abrahamu,+ Isaka,+ na Israeli, acha leo ijulikane kwamba wewe ni Mungu katika Israeli na kwamba mimi ni mtumishi wako na kwamba nimefanya mambo haya yote kwa neno lako.+ 37 Nijibu, Ee Yehova! Nijibu ili watu hawa wajue kwamba wewe, Yehova, ndiye Mungu wa kweli na kwamba wewe unaigeuza mioyo yao ikurudie.”+

38 Ndipo moto wa Yehova ukashuka kutoka juu, ukaiteketeza hiyo dhabihu ya kuteketezwa,+ kuni, mawe, na mavumbi, nao ukayaramba maji yaliyokuwa mtaroni.+ 39 Watu wote walipoona jambo hilo, mara moja wakaanguka chini kifudifudi na kusema: “Yehova ndiye Mungu wa kweli! Yehova ndiye Mungu wa kweli!” 40 Kisha Eliya akawaambia: “Wakamateni manabii wa Baali! Msimwache hata mmoja wao atoroke!” Mara moja wakawakamata, na Eliya akawaleta chini kwenye kijito cha* Kishoni+ na kuwachinja huko.+

41 Sasa Eliya akamwambia Ahabu: “Panda juu, ukale na kunywa, kwa maana kuna sauti ya mvua kubwa sana.”+ 42 Basi Ahabu akapanda juu kwenda kula na kunywa, lakini Eliya akapanda kwenye kilele cha Karmeli, akajikunyata ardhini, uso wake ukiwa katikati ya magoti yake.+ 43 Kisha akamwambia mtumishi wake: “Panda juu, tafadhali, utazame upande wa bahari.” Basi akapanda juu, akatazama na kusema: “Hakuna kitu chochote.” Eliya akamwambia mara saba, “Rudi.” 44 Mara ya saba mtumishi wake akamwambia: “Tazama! Kuna wingu dogo kama mkono wa mwanadamu linalopanda kutoka baharini.” Ndipo Eliya akasema: “Nenda, mwambie hivi Ahabu: ‘Funga farasi kwenye gari! Teremka ili mvua kubwa isikuzuie!’” 45 Wakati huo, mawingu mazito yakatanda angani, upepo ukavuma, na mvua kubwa sana ikanyesha;+ naye Ahabu akaendesha gari mpaka Yezreeli.+ 46 Lakini mkono wa Yehova ukaja juu ya Eliya, akajifunga vazi lake kiunoni, akakimbia na kumpita Ahabu na kutangulia kufika Yezreeli.

19 Kisha Ahabu+ akamwambia Yezebeli+ mambo yote ambayo Eliya alikuwa amefanya na jinsi alivyowaua manabii wote kwa upanga.+ 2 Ndipo Yezebeli akamtuma mjumbe kwa Eliya, akisema: “Miungu na iniadhibu, tena vikali, ikiwa kufikia kesho wakati kama huu sitakufanya uwe kama* kila mmoja wa manabii hao!” 3 Basi Eliya akaogopa, akaondoka na kukimbia ili kuokoa uhai wake.*+ Akafika Beer-sheba,+ jiji la Yuda,+ akamwacha mtumishi wake huko. 4 Akaingia nyikani safari ya siku moja, akafika na kuketi chini ya mti wa mretemu, naye akaomba afe. Akasema: “Imetosha! Sasa, Ee Yehova, niue,*+ kwa sababu mimi si bora kuliko mababu zangu.”

5 Kisha akalala chini na kushikwa na usingizi chini ya mti huo wa mretemu. Lakini kwa ghafla malaika akamgusa+ na kumwambia: “Amka, ule.”+ 6 Alipoangalia, aliona karibu na kichwa chake mkate wa mviringo ukiwa juu ya mawe yenye moto na pia gudulia la maji. Akala na kunywa na kulala chini tena. 7 Baadaye malaika wa Yehova akarudi mara ya pili, akamgusa na kusema: “Amka, ule, kwa maana safari itakuwa ngumu sana kwako.” 8 Basi akaamka, akala na kunywa, na kwa nguvu za chakula hicho akasafiri kwa siku 40, mchana na usiku, mpaka alipofika Horebu, mlima wa Mungu wa kweli.+

9 Huko akaingia pangoni+ na kulala humo usiku; na tazama! neno la Yehova likamjia na kumuuliza: “Unafanya nini hapa, Eliya?” 10 Akajibu: “Nimekuwa na bidii kwelikweli kwa ajili ya Yehova Mungu wa majeshi;+ kwa maana Waisraeli wameliacha agano lako,+ wamebomoa madhabahu zako, na kuwaua manabii wako kwa upanga,+ nimebaki mimi peke yangu. Sasa wanataka kuniua.”*+ 11 Lakini Akasema: “Toka nje, ukasimame mlimani mbele za Yehova.” Na tazama! Yehova alikuwa akipita karibu,+ na upepo mkali na wenye nguvu ulikuwa ukipasua milima na kuvunja miamba mbele za Yehova,+ lakini Yehova hakuwa katika upepo huo. Baada ya upepo, kukawa na tetemeko la ardhi,+ lakini Yehova hakuwa katika tetemeko hilo. 12 Baada ya tetemeko la ardhi, kukawa na moto,+ lakini Yehova hakuwa katika moto huo. Baada ya moto, kukawa na sauti tulivu, ya chini.+ 13 Mara tu Eliya alipoisikia, aliufunika uso wake kwa vazi lake rasmi,+ akatoka nje na kusimama kwenye mlango wa pango. Kisha sauti ikamuuliza: “Unafanya nini hapa, Eliya?” 14 Akasema: “Nimekuwa na bidii kwelikweli kwa ajili ya Yehova Mungu wa majeshi; kwa maana Waisraeli wameliacha agano lako,+ wamebomoa madhabahu zako, na kuwaua manabii wako kwa upanga, nimebaki mimi peke yangu. Sasa wanataka kuniua.”*+

15 Yehova akamwambia: “Rudi, nenda katika nyika ya Damasko. Utakapofika huko, mtie mafuta Hazaeli+ awe mfalme wa Siria. 16 Pia unapaswa kumtia mafuta Yehu+ mjukuu wa Nimshi awe mfalme wa Israeli, na umtie mafuta Elisha mwana wa Shafati kutoka Abel-mehola awe nabii baada yako.+ 17 Mtu yeyote atakayeponyoka upanga wa Hazaeli,+ Yehu atamuua;+ na yeyote atakayeponyoka upanga wa Yehu, Elisha atamuua.+ 18 Na bado nina watu 7,000 waliobaki Israeli,+ watu wote ambao hawakumpigia magoti Baali,+ na ambao hawakumbusu kwa midomo yao.”+

19 Basi akaondoka huko, akamkuta Elisha mwana wa Shafati akilima kwa jozi 12 za ng’ombe dume, naye alikuwa na jozi ya 12. Basi Eliya akamkaribia, akalitupa vazi lake rasmi+ juu yake. 20 Ndipo akawaacha wale ng’ombe dume, akamfuata Eliya mbio na kusema: “Tafadhali, niruhusu nimbusu baba yangu na mama yangu. Kisha nitakufuata.” Eliya akamwambia: “Nenda, rudi nyumbani, nimekuzuia kwa njia gani?” 21 Basi akarudi, akachukua jozi moja ya ng’ombe dume na kuwatoa dhabihu, naye akatumia vifaa vya kulimia kuchemsha nyama ya ng’ombe dume hao, kisha akawapa watu, nao wakala. Baada ya hapo akaondoka na kumfuata Eliya na kuanza kumhudumia.+

20 Basi Mfalme Ben-hadadi+ wa Siria+ akakusanya jeshi lake lote pamoja na wafalme wengine 32 wakiwa na farasi wao na magari yao ya vita; akapanda kwenda kuzingira+ jiji la Samaria+ na kupigana nalo. 2 Kisha akawatuma wajumbe kwa Mfalme Ahabu+ wa Israeli jijini, akamwambia: “Ben-hadadi anasema, 3 ‘Fedha yako na dhahabu yako ni yangu, na pia wake zako warembo zaidi na wana wako ni wangu.’” 4 Ndipo mfalme wa Israeli akasema: “Kama ulivyosema bwana wangu mfalme, mimi ni wako pamoja na vitu vyangu vyote.”+

5 Baadaye wajumbe hao wakarudi na kusema: “Ben-hadadi anasema, ‘Nilituma ujumbe huu kwako: “Utanipa fedha yako, dhahabu yako, wake zako, na wana wako.” 6 Lakini kesho wakati kama huu nitawatuma watumishi wangu kwako, nao wataichunguza kwa makini nyumba yako na nyumba za watumishi wako, watachukua vitu vyako vyote vinavyotamanika na kwenda navyo.’”

7 Ndipo mfalme wa Israeli akawaita wazee wote wa nchi na kuwaambia: “Angalieni, tafadhali, na mjue kwamba mtu huyu anakusudia kuleta msiba, kwa maana alitaka nimpe wake zangu, wanangu, fedha yangu, na dhahabu yangu, nami sikukataa agizo lake.” 8 Ndipo wazee wote na watu wote wakamwambia: “Usitii, wala kukubali.” 9 Kwa hiyo akawaambia wajumbe wa Ben-hadadi: “Mwambieni bwana wangu mfalme, ‘Mambo yote ambayo ulitaka mwanzoni mimi mtumishi wako nifanye nitafanya, lakini siwezi kufanya jambo hili.’” Basi wajumbe hao wakaenda zao, wakampelekea ujumbe huo.

10 Kisha Ben-hadadi akatuma ujumbe huu kwake: “Miungu na iniadhibu, tena vikali, ikiwa kuna mavumbi ya kutosha Samaria hivi kwamba kila mtu anayenifuata anaweza kupata konzi moja!” 11 Mfalme wa Israeli akajibu hivi: “Mwambieni, ‘Anayevaa silaha zake hapaswi kujigamba kama mtu anayezivua.’”+ 12 Mara tu Ben-hadadi aliposikia jibu hilo, yeye na wale wafalme walipokuwa wakinywa katika mahema yao,* akawaambia watumishi wake: “Jitayarisheni kushambulia!” Basi wakajitayarisha kushambulia jiji hilo.

13 Lakini nabii fulani akaenda kwa Mfalme Ahabu+ wa Israeli na kumwambia: “Yehova anasema, ‘Je, umeuona umati huu wote mkubwa? Tazama, ninautia mikononi mwako leo, kisha utajua kwamba mimi ni Yehova.’”+ 14 Ahabu akauliza: “Kupitia nani?” Nabii huyo akasema: “Yehova anasema hivi: ‘Kupitia watumishi wa wakuu wa mikoa.’”* Ndipo Ahabu akamuuliza: “Ni nani atakayeanzisha vita?” Nabii huyo akasema: “Ni wewe!”

15 Kisha Ahabu akawahesabu watumishi wa wakuu wa mikoa, nao walikuwa 232; halafu akawahesabu wanaume wote wa Israeli, walikuwa 7,000. 16 Wakaondoka wakati wa adhuhuri Ben-hadadi alipokuwa akinywa na kulewa katika mahema* pamoja na wale wafalme 32 waliokuwa wakimsaidia. 17 Watumishi wa wakuu wa mikoa walipotoka kwanza, mara moja Ben-hadadi akawatuma wajumbe. Wakamletea habari hii: “Wanaume wamekuja kutoka Samaria.” 18 Ndipo akasema: “Ikiwa wamekuja kwa amani, waleteni wakiwa hai; ikiwa wamekuja kwa ajili ya vita, bado mnapaswa kuwaleta wakiwa hai.” 19 Lakini watu hao walipotoka jijini—watumishi wa wakuu wa mikoa na majeshi yaliyokuwa yakiwafuata— 20 kila mmoja wao akamuua adui yake. Ndipo Wasiria wakakimbia,+ na Waisraeli wakawafuatia, lakini Mfalme Ben-hadadi wa Siria akapanda farasi na kutoroka pamoja na baadhi ya wapanda farasi. 21 Lakini mfalme wa Israeli akatoka na kuendelea kuwaua maadui waliopanda farasi na magari, naye akapata ushindi mkubwa dhidi ya Wasiria.*

22 Baadaye nabii huyo+ akaenda kwa mfalme wa Israeli na kumwambia: “Nenda, jiimarishe na ufikirie jambo utakalofanya,+ kwa maana mwanzoni mwa mwaka ujao* mfalme wa Siria atakuja kukushambulia.”+

23 Sasa watumishi wa mfalme wa Siria wakamwambia: “Mungu wao ni Mungu wa milima. Ndiyo sababu walitushinda nguvu. Lakini tukipigana nao kwenye nchi tambarare, tutawashinda nguvu. 24 Fanya hivi pia: Waondoe wafalme wote+ katika nafasi zao, na mahali pao uweke magavana. 25 Kisha ukusanye* jeshi linalolingana na jeshi ulilopoteza, farasi kwa farasi na gari kwa gari. Acha tupigane nao kwenye nchi tambarare, na hakika tutawashinda nguvu.” Basi akasikiliza ushauri wao na kufanya kama walivyosema.

26 Mwanzoni mwa mwaka,* Ben-hadadi akawakusanya Wasiria, akapanda kwenda Afeki+ ili kupigana na Waisraeli. 27 Waisraeli pia walikusanywa kwa ajili ya vita na kupewa vitu walivyohitaji, nao wakatoka kwenda kukabiliana nao. Waisraeli walipopiga kambi mbele yao, walikuwa kama vikundi viwili vidogo vya mbuzi, lakini Wasiria walijaa kote nchini.+ 28 Kisha yule mtu wa Mungu wa kweli akaenda kwa mfalme wa Israeli na kumwambia: “Yehova anasema hivi, ‘Kwa sababu Wasiria wamesema: “Yehova ni Mungu wa milima, wala si Mungu wa nchi tambarare,” nitautia umati huu wote mkubwa mkononi mwako,+ na hakika utajua kwamba mimi ni Yehova.’”+

29 Wakaendelea kupiga kambi wakielekeana kwa siku saba, na katika siku ya saba vita vikaanza. Kwa siku moja, Waisraeli wakawaua wanajeshi 100,000 Wasiria wanaotembea kwa miguu. 30 Wanajeshi waliobaki wakakimbilia Afeki,+ ndani ya jiji. Lakini ukuta ukawaangukia wanaume 27,000 kati ya wale waliokuwa wamebaki. Ben-hadadi pia akakimbia na kuingia jijini, akajificha katika chumba fulani cha ndani.

31 Kwa hiyo watumishi wake wakamwambia: “Tazama, tumesikia kwamba wafalme wa nyumba ya Israeli ni wafalme wenye rehema.* Tafadhali, turuhusu tuvae nguo za magunia viunoni na kufunga kamba vichwani kisha twende kwa mfalme wa Israeli. Huenda akakuacha hai.”*+ 32 Basi wakavaa nguo za magunia viunoni na kufunga kamba vichwani, wakaenda kwa mfalme wa Israeli na kumwambia: “Mtumishi wako Ben-hadadi anasema, ‘Tafadhali, niruhusu niishi.’”* Akasema: “Je, angali hai? Yeye ni ndugu yangu.” 33 Basi watu hao wakaliona jambo hilo kuwa ishara njema, na bila kukawia wakaamini maneno yake, wakamwambia: “Ben-hadadi ni ndugu yako.” Kwa hiyo akasema: “Nendeni mkamlete.” Kisha Ben-hadadi akatoka na kwenda kwake, mfalme akampandisha garini.

34 Sasa Ben-hadadi akamwambia: “Majiji ambayo baba yangu alichukua kutoka kwa baba yako nitayarudisha, nawe unaweza kujianzishia masoko* Damasko, kama baba yangu alivyofanya Samaria.”

Ahabu akamwambia, “Kwa msingi wa makubaliano haya,* nitakuruhusu uende.”

Basi akafanya makubaliano naye na kumruhusu aende zake.

35 Kwa neno la Yehova, mmoja wa wana wa manabii*+ akamwambia mwenzake: “Tafadhali, nipige.” Lakini mtu huyo akakataa kumpiga. 36 Basi akamwambia: “Kwa sababu hukuisikiliza sauti ya Yehova, mara tu tutakapoachana, simba atakuua.” Walipoachana, simba akatokea na kumuua.

37 Akamkuta mtu mwingine na kumwambia: “Tafadhali, nipige.” Mtu huyo akampiga na kumjeruhi.

38 Kisha nabii huyo akaenda na kumsubiri mfalme kando ya barabara, akafunika macho yake kwa kitambaa ili aufiche uso wake. 39 Mfalme alipokuwa akipita, akamlilia mfalme akisema: “Mimi mtumishi wako nilienda sehemu ambayo mapambano yalikuwa makali vitani, na mtu fulani alikuwa akitoka vitani akaniletea mwanamume mmoja na kuniambia, ‘Mlinde mtu huyu. Akitoroka, utalipia uhai wake kwa uhai wako,*+ la sivyo utalipa talanta moja* ya fedha.’ 40 Na mimi mtumishi wako nilipokuwa nikishughulika hapa na pale, kwa ghafla mtu huyo akatoroka.” Mfalme wa Israeli akamwambia: “Hivyo ndivyo utakavyohukumiwa; umejihukumu mwenyewe.” 41 Kisha akaondoa haraka kitambaa kilichofunika macho yake, na mfalme wa Israeli akatambua kwamba alikuwa mmoja wa manabii.+ 42 Mtu huyo akamwambia mfalme: “Yehova anasema hivi: ‘Kwa sababu umemwacha atoroke kutoka mikononi mwako mtu ambaye nilisema anapaswa kuuawa,+ utalipia uhai wake kwa uhai wako,*+ na watu wako watachukua mahali pa watu wake.’”+ 43 Ndipo mfalme wa Israeli akaenda nyumbani Samaria,+ akiwa amesononeka na kuvunjika moyo.

21 Baada ya hayo, jambo fulani lilitendeka kuhusiana na shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli; lilikuwa Yezreeli,+ kando ya jumba la Mfalme Ahabu, mfalme wa Samaria. 2 Ahabu akamwambia Nabothi: “Nipe shamba lako la mizabibu ili nilifanye kuwa shamba la mboga, kwa sababu liko karibu na nyumba yangu. Badala ya shamba hilo, nitakupa shamba bora zaidi la mizabibu. Au ukipenda, nitakulipa pesa zinazolingana na thamani yake.” 3 Lakini Nabothi akamwambia Ahabu: “Ni jambo nisiloweza kamwe kuwazia, kulingana na maoni ya Yehova, kukupa urithi wa mababu zangu.”+ 4 Basi Ahabu akaingia nyumbani mwake, akiwa amesononeka na kuvunjika moyo kwa sababu ya jibu ambalo Nabothi Myezreeli alimpa aliposema: “Sitakupa urithi wa mababu zangu.” Kisha akalala kitandani mwake, akaugeuzia mbali uso wake, na kukataa kula.

5 Yezebeli mke wake+ akaingia ndani kumwona, akamuuliza, “Kwa nini umehuzunika* sana hivi kwamba unakataa kula?” 6 Akamjibu: “Ni kwa sababu nilimwambia Nabothi Myezreeli, ‘Niuzie shamba lako la mizabibu. Au ukipenda, nitakupa shamba lingine la mizabibu badala ya shamba hilo.’ Lakini akaniambia, ‘Sitakupa shamba langu la mizabibu.’” 7 Yezebeli mke wake akamwambia: “Je, si wewe unayetawala ukiwa mfalme wa Israeli? Inuka, kula chakula, moyo wako na uchangamke. Nitakupa shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli.”+ 8 Basi Yezebeli akaandika barua kwa jina la Ahabu, akazipiga muhuri wa Ahabu+ na kuzituma barua hizo kwa wazee+ na wakuu walioishi katika jiji la Nabothi. 9 Aliandika hivi katika barua hizo: “Tangazeni watu wafunge, halafu mketisheni Nabothi mbele ya watu. 10 Nanyi muwaketishe watu wawili wasiofaa kitu mbele yake ili watoe ushahidi dhidi yake,+ wakisema, ‘Umemtukana Mungu na mfalme!’+ Kisha mtoeni nje na kumuua kwa kumpiga mawe.”+

11 Basi watu wa jiji lake, wazee na wakuu walioishi katika jiji lake, wakafanya kama ilivyoandikwa katika barua ambazo Yezebeli aliwatumia. 12 Wakatangaza watu wafunge, kisha wakamketisha Nabothi mbele ya watu. 13 Ndipo watu wawili miongoni mwa watu wasiofaa kitu wakaja na kuketi mbele yake, nao wakaanza kutoa ushahidi dhidi ya Nabothi mbele ya watu, wakisema: “Nabothi amemtukana Mungu na mfalme!”+ Kisha wakamtoa nje ya jiji, wakamuua kwa kumpiga mawe.+ 14 Halafu wakamtumia Yezebeli ujumbe huu: “Nabothi ameuawa kwa kupigwa mawe.”+

15 Mara tu Yezebeli aliposikia kwamba Nabothi amepigwa mawe akafa, akamwambia Ahabu: “Inuka, chukua shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli,+ ambalo alikataa kukuuzia, kwa maana Nabothi hayuko hai tena. Amekufa.” 16 Mara tu Ahabu aliposikia kwamba Nabothi amekufa, Ahabu aliondoka, akashuka kwenda kwenye shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli ili alichukue.

17 Lakini neno la Yehova likamjia Eliya+ Mtishbi, likisema: 18 “Ondoka, nenda ukutane na Ahabu mfalme wa Israeli huko Samaria.+ Yuko katika shamba la mizabibu la Nabothi, ameenda huko kulichukua. 19 Mwambie hivi: ‘Yehova anauliza hivi: “Je, umemuua mtu+ na kuchukua mali yake?”’+ Kisha mwambie, ‘Yehova anasema hivi: “Mahali ambapo mbwa waliramba damu ya Nabothi, ndipo watakapoiramba damu yako mwenyewe.”’”+

20 Ahabu akamwambia Eliya: “Yaani umenipata, ewe adui yangu?”+ Akajibu: “Nimekupata. ‘Kwa sababu umeazimia* kutenda maovu machoni pa Yehova,+ 21 sasa ninakuletea msiba, nami nitafagia kabisa baada yako na kumwangamiza kila mwanamume* wa Ahabu,+ kutia ndani wasio na uwezo na walio dhaifu katika Israeli.+ 22 Nami nitaifanya nyumba yako iwe kama nyumba ya Yeroboamu+ mwana wa Nebati na kama nyumba ya Baasha+ mwana wa Ahiya, kwa sababu umenikasirisha na kusababisha Waisraeli watende dhambi.’ 23 Pia Yehova anasema hivi kumhusu Yezebeli: ‘Mbwa watamla Yezebeli katika shamba la Yezreeli.+ 24 Mtu yeyote wa Ahabu anayefia jijini mbwa watamla, na yeyote anayefia shambani ndege wa angani watamla.+ 25 Kwa kweli, hajawahi kamwe kutokea mtu yeyote kama Ahabu,+ aliyeazimia kabisa* kutenda maovu machoni pa Yehova, akichochewa na Yezebeli mke wake.+ 26 Alitenda kwa njia yenye kuchukiza kabisa kwa kufuata sanamu zenye kuchukiza,* kama Waamori wote walivyokuwa wamefanya, ambao Yehova aliwafukuza kutoka mbele ya Waisraeli.’”+

27 Mara tu Ahabu aliposikia maneno hayo, akararua mavazi yake na kuvaa nguo za magunia; akaanza kufunga na kulala chini katika nguo za magunia na kutembea kwa huzuni. 28 Kisha neno hili la Yehova likamjia Eliya Mtishbi: 29 “Je, umeona jinsi ambavyo Ahabu amejinyenyekeza kwa sababu yangu?+ Kwa sababu amejinyenyekeza mbele zangu, sitauleta msiba huo akiwa hai. Nitailetea nyumba yake msiba huo katika siku za mwanawe.”+

22 Kwa miaka mitatu hakukuwa na vita kati ya Siria na Israeli. 2 Katika mwaka wa tatu, Mfalme Yehoshafati+ wa Yuda akashuka kwenda kwa mfalme wa Israeli.+ 3 Kisha mfalme wa Israeli akawaambia watumishi wake: “Je, mnajua kwamba Ramothi-gileadi+ ni jiji letu? Na bado tunasitasita kulichukua kutoka kwa mfalme wa Siria.” 4 Halafu akamuuliza Yehoshafati: “Je, utaenda pamoja nami kupigana kule Ramothi-gileadi?” Yehoshafati akamjibu hivi mfalme wa Israeli: “Mimi ni kama wewe. Watu wangu ni kama watu wako. Farasi wangu ni kama farasi wako.”+

5 Lakini Yehoshafati akamwambia mfalme wa Israeli: “Tafadhali, kwanza tafuta+ neno la Yehova.”+ 6 Kwa hiyo mfalme wa Israeli akawakusanya pamoja manabii, wanaume wapatao 400, akawauliza: “Je, niende kupigana vita dhidi ya Ramothi-gileadi, au nisiende?” Wakasema: “Panda uende, na Yehova atalitia jiji hilo mikononi mwako.”

7 Kisha Yehoshafati akasema: “Je, hakuna nabii wa Yehova mahali hapa? Acheni tumuulize yeye pia.”+ 8 Ndipo mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati: “Bado kuna mtu mmoja ambaye tunaweza kumwomba ushauri kutoka kwa Yehova;+ lakini ninamchukia,+ kwa maana hatabiri kamwe mambo mema kunihusu, ila mabaya tu.+ Anaitwa Mikaya mwana wa Imla.” Hata hivyo, Yehoshafati akasema: “Mfalme, usiseme jambo kama hilo.”

9 Basi mfalme wa Israeli akamwita ofisa fulani wa makao ya mfalme na kumwambia: “Mlete haraka Mikaya mwana wa Imla.”+ 10 Sasa mfalme wa Israeli na Yehoshafati mfalme wa Yuda walikuwa wameketi kila mmoja wao kwenye kiti chake cha ufalme, akiwa amevaa mavazi ya kifalme, katika uwanja wa kupuria nafaka kwenye lango la kuingia Samaria, na manabii wote walikuwa wakitabiri mbele yao.+ 11 Kisha Sedekia mwana wa Kenaana akajitengenezea pembe za chuma na kusema: “Yehova anasema hivi: ‘Kwa pembe hizi utawapiga* Wasiria mpaka utakapowaangamiza.’” 12 Wale manabii wengine wote walikuwa wakitabiri vivyo hivyo, wakisema: “Panda mpaka Ramothi-gileadi, nawe utafanikiwa; Yehova atalitia jiji hilo mikononi mwako mfalme.”

13 Basi mjumbe aliyeenda kumwita Mikaya akamwambia: “Tazama! Manabii wote kwa pamoja wanasema mema kumhusu mfalme. Tafadhali, acha neno lako liwe kama maneno yao, useme mema.”+ 14 Lakini Mikaya akasema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, jambo lolote ambalo Yehova ataniambia ndilo nitakalosema.” 15 Kisha akaingia kwa mfalme, naye mfalme akamuuliza: “Mikaya, je, twende kupigana vita dhidi ya Ramothi-gileadi, au tusiende?” Mara moja akajibu: “Panda uende nawe utafanikiwa; Yehova atalitia jiji hilo mikononi mwako.” 16 Ndipo mfalme akamuuliza: “Nitakuapisha mara ngapi kwamba hupaswi kuniambia jambo lingine lolote isipokuwa ukweli katika jina la Yehova?” 17 Basi Mikaya akasema: “Ninawaona Waisraeli wote wakiwa wametawanyika milimani,+ kama kondoo wasio na mchungaji. Yehova akasema: ‘Hawa hawana bwana. Acha kila mmoja wao arudi kwa amani nyumbani kwake.’”

18 Kisha mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati: “Je, sikukwambia, ‘Hatatabiri mambo mema kunihusu, ila mabaya’?”+

19 Ndipo Mikaya akasema: “Basi, sikia neno la Yehova: Nilimwona Yehova akiwa ameketi kwenye kiti chake cha ufalme+ na jeshi lote la mbinguni likiwa limesimama kando yake, upande wake wa kulia na upande wake wa kushoto.+ 20 Halafu Yehova akauliza, ‘Ni nani atakayemdanganya Ahabu, ili apande kwenda na kufia huko Ramothi-gileadi?’ Na malaika mmoja akasema jambo moja na mwingine akasema jambo lingine. 21 Kisha roho*+ fulani akaja na kusimama mbele za Yehova na kusema, ‘Mimi nitamdanganya.’ Yehova akamuuliza, ‘Utatumia njia gani?’ 22 Akajibu, ‘Nitaenda na kuwa roho ya udanganyifu katika vinywa vya manabii wake wote.’+ Kwa hiyo akasema, ‘Utamdanganya, na zaidi ya hilo, utafanikiwa. Nenda ukafanye hivyo.’ 23 Na sasa Yehova ametia roho ya udanganyifu katika vinywa vya hawa manabii wako wote,+ lakini Yehova ametangaza kwamba utapata msiba.”+

24 Sasa Sedekia mwana wa Kenaana akamkaribia Mikaya na kumpiga kwenye shavu na kumuuliza: “Roho ya Yehova iliniacha jinsi gani na kuja kuzungumza nawe?”+ 25 Mikaya akamjibu: “Tazama! Utajua ni jinsi gani utakapoingia katika chumba cha ndani zaidi kujificha.” 26 Ndipo mfalme wa Israeli akasema: “Mchukue Mikaya umpeleke kwa Amoni mkuu wa jiji na kwa Yoashi mwana wa mfalme. 27 Waambie, ‘Mfalme anasema hivi: “Mfungeni mtu huyu gerezani+ na kumlisha kiasi kidogo cha mkate na maji mpaka nitakaporudi kwa amani.”’” 28 Lakini Mikaya akasema: “Ukirudi kwa amani, basi Yehova hajazungumza nami.”+ Kisha akasema: “Zingatieni maneno yangu, enyi watu wote.”

29 Basi mfalme wa Israeli na Yehoshafati mfalme wa Yuda wakapanda kwenda Ramothi-gileadi.+ 30 Ndipo mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati: “Nitabadili sura yangu na kuingia vitani, lakini wewe vaa mavazi yako ya kifalme.” Kwa hiyo mfalme wa Israeli akabadili sura yake+ na kuingia vitani. 31 Sasa mfalme wa Siria alikuwa amewaagiza hivi makamanda wake 32 wa magari ya vita:+ “Msipigane na yeyote, mdogo au mkubwa, isipokuwa mfalme wa Israeli.” 32 Na mara tu makamanda hao wa magari ya vita walipomwona Yehoshafati, wakaambiana: “Hakika huyu ndiye mfalme wa Israeli.” Basi wakamgeukia ili kupigana naye; na Yehoshafati akaanza kulilia msaada. 33 Makamanda hao wa magari ya vita walipoona kwamba hakuwa mfalme wa Israeli, mara moja wakaacha kumfuatia.

34 Lakini mtu fulani alivuta upinde wake bila kukusudia na kumpiga mfalme wa Israeli katikati ya sehemu ambazo koti lake la vita linaungana. Basi mfalme akamwambia mtu aliyeendesha gari lake: “Geuka uniondoe vitani,* kwa sababu nimejeruhiwa vibaya.”+ 35 Vita vikapamba moto siku hiyo yote, nao wakalazimika kumsimamisha mfalme ndani ya gari akiwaelekea Wasiria. Damu ya jeraha lake ikamwagika ndani ya gari lake la vita, akafa jioni.+ 36 Jua lilipokuwa likitua amri hii ikatangazwa kambini: “Kila mtu aende katika jiji lake! Kila mtu aende katika nchi yake!”+ 37 Basi mfalme akafa, akaletwa Samaria; wakamzika mfalme huko Samaria. 38 Walipolisafisha gari hilo la vita kando ya kidimbwi cha Samaria, mbwa waliramba damu yake na makahaba wakaogea mahali hapo,* kama Yehova alivyokuwa amesema.+

39 Na mambo mengine katika historia ya Ahabu, mambo yote aliyofanya na nyumba aliyojenga ya* pembe za tembo+ na majiji yote aliyojenga, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli? 40 Kisha Ahabu akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake;+ na Ahazia+ mwana wake akawa mfalme baada yake.

41 Yehoshafati+ mwana wa Asa aliwekwa kuwa mfalme wa Yuda katika mwaka wa nne wa utawala wa Mfalme Ahabu wa Israeli. 42 Yehoshafati alikuwa na umri wa miaka 35 alipowekwa kuwa mfalme, naye alitawala kwa miaka 25 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Azuba binti ya Shilhi. 43 Yehoshafati aliendelea kutembea katika njia yote ya Asa+ baba yake. Hakugeuka na kuiacha njia hiyo, naye alitenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova.+ Hata hivyo, mahali pa juu hapakuondolewa, na bado watu walikuwa wakitoa dhabihu na kufukiza moshi wa dhabihu mahali pa juu.+ 44 Yehoshafati alidumisha mahusiano ya amani na mfalme wa Israeli.+ 45 Na mambo mengine katika historia ya Yehoshafati, mambo makuu aliyotekeleza na jinsi alivyopigana vita, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda? 46 Pia aliwaondoa kabisa nchini wanaume wote makahaba wa hekaluni+ waliobaki katika siku za Asa baba yake.+

47 Wakati huo hakukuwa na mfalme katika nchi ya Edomu;+ naibu ndiye aliyetawala kama mfalme.+

48 Yehoshafati pia akatengeneza meli* za Tarshishi za kwenda Ofiri kuleta dhahabu,+ lakini hazikwenda kwa sababu meli hizo zilivunjika huko Esion-geberi.+ 49 Wakati huo ndipo Ahazia mwana wa Ahabu alipomwambia Yehoshafati: “Waruhusu watumishi wangu wasafiri na watumishi wako katika meli hizo,” lakini Yehoshafati hakukubali.

50 Kisha Yehoshafati akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake+ katika Jiji la Daudi babu yake; na Yehoramu+ mwanawe akawa mfalme baada yake.

51 Ahazia+ mwana wa Ahabu akawa mfalme wa Israeli huko Samaria katika mwaka wa 17 wa utawala wa Mfalme Yehoshafati wa Yuda, naye alitawala Israeli kwa miaka miwili. 52 Aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova na kutembea katika njia ya baba yake+ na mama yake+ na katika njia ya Yeroboamu mwana wa Nebati, aliyesababisha Waisraeli watende dhambi.+ 53 Aliendelea kumwabudu Baali+ na kumwinamia, akaendelea kumkasirisha Yehova Mungu wa Israeli,+ kama baba yake alivyokuwa amefanya.

Tnn., “siku zake zilikuwa zimesonga.”

Au “kumuumiza hisia.”

Au “nafsi yako mwenyewe na nafsi ya.”

Au “aliyeikomboa nafsi yangu.”

Au “nyumbu jike.”

Au “anayeheshimiwa.”

Tnn., “Ninafuata njia ya dunia yote.”

Tnn., “maamuzi yake.”

Au “utakapotenda kwa hekima.”

Angalia Kamusi.

Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.

Tnn., “usiruhusu mvi zake zishuke kwa amani Kaburini.”

Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.

Tnn., “ni lazima ushushe mvi zake Kaburini pamoja na damu.”

Au “dhidi ya nafsi yake.”

Au “ukoo wa kifalme.”

Tnn., “atarudisha damu yake juu ya kichwa chake mwenyewe.”

Au “wazao.”

Au “wazao.”

Tnn., “ataleta madhara hayo juu ya kichwa chako mwenyewe.”

Au “Alimchukua.”

Tnn., “pakuu.”

Au “mvulana mdogo.”

Tnn., “na sijui kutoka nje na kuingia ndani.”

Au labda, “wagumu.” Tnn., “wazito.”

Tnn., “siku nyingi.”

Tnn., “siku zako zote.”

Tnn., “nitarefusha siku zako.”

Tnn., “kifuani pake.”

Au “wakuu wake.”

Kori moja ilikuwa sawa na lita 220 (kilogramu 170 hivi). Angalia Nyongeza B14.

Yaani, upande wa magharibi wa Mto Efrati.

Idadi hii inapatikana katika baadhi ya hati na pia katika simulizi lingine kama hili. Hati nyingine zinasema mabanda hayo yalikuwa 40,000.

Au “wapanda farasi.”

Au “Alinena.”

Au “viumbe wanaoruka.”

Huenda viumbe hao walitia ndani wanyama wanaotambaa na wadudu.

Au “alimpenda Daudi.”

Au “lenye watu wengi sana.”

Kori moja ilikuwa sawa na lita 220 (kilogramu 170 hivi). Angalia Nyongeza B14.

Tnn., “za mafuta yaliyopondwapondwa.”

Au “agano.”

Au “wabeba mizigo.”

Tnn., “wana wa Israeli.”

Angalia Nyongeza B15.

Angalia Nyongeza B8.

Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.

Tnn., “hekalu la nyumba.”

Au “upana.”

Yaani, Patakatifu.

Tnn., “kulia.”

Tnn., “maamuzi yangu.”

Yaani, ndani ya nyumba hiyo.

Yaani, Patakatifu, palipokuwa mbele ya Patakatifu Zaidi.

Tnn., “mti wa mafuta,” labda ni msonobari wa Aleppo.

Yaani, Patakatifu Zaidi.

Huenda inarejelea ujenzi wa kiunzi cha mlango au ukubwa wa milango.

Yaani, Patakatifu.

Huenda inarejelea ujenzi wa kiunzi cha mlango au ukubwa wa milango.

Angalia Nyongeza B15.

Angalia Nyongeza B15.

Au “jumba lake la mfalme.”

Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.

Au “mstatili.”

Au “Jumba la mfalme.”

Tnn., “nyumba ya Ukumbi.”

Au “na kila moja ya nguzo hizo mbili ilikuwa na mzingo wa mikono 12.”

Yaani, Patakatifu.

Au “ya kusini.”

Maana yake “Naye [yaani, Yehova] Aimarishe Kabisa.”

Au “ya kaskazini.”

Labda inamaanisha “Katika Nguvu.”

Au “tangi.”

Au “ilikuwa na mzingo wa mikono 30.”

Karibu sentimita 7.4 (inchi 2.9). Angalia Nyongeza B14.

Bathi ilikuwa sawa na lita 22. Angalia Nyongeza B14.

Au “mikokoteni kumi ya maji.”

Au “tindi.”

Au “zilikuwa kipande kimoja na gari hilo.”

Au “zikiwa kipande kimoja na gari hilo.”

Au “kipenyo cha mikono minne.”

Yaani, ukoo wa upande wa baba.

Yaani, Sherehe ya Vibanda.

Angalia Nyongeza B15.

Tnn., “mwana wako, atakayetoka katika viuno vyako.”

Au “aliyetendewa dhambi akimweka chini ya laana.” Yaani, kiapo kinacholeta laana ikiwa mtu anaapa kwa uwongo au kukosa kutimiza kiapo hicho.

Tnn., “laana.”

Tnn., “laana.”

Tnn., “kuleta juu ya kichwa chake mwenyewe jambo alilotenda.”

Tnn., “kuwa mwadilifu.”

Au “umewatesa.”

Au “panzi.”

Tnn., “katika nchi ya malango yake.”

Au “sifa yako.”

Angalia Kamusi.

Tnn., “Utawafanya wawe vitu vya kuhurumiwa mbele ya waliowateka.”

Au “kuwasikiliza wanapokuomba jambo lolote.”

Tnn., “maamuzi yake.”

Au “imtumikie kikamili.”

Au “njia ya kuingia Hamathi.”

Angalia Kamusi.

Tnn., “Siku ya nane,” yaani, siku iliyofuata kipindi cha pili cha siku saba.

Au “jumba la mfalme.”

Tnn., “hukumu.”

Tnn., “methali.”

Au “jumba la.”

Tnn., “hayakuwa sawa machoni pake.”

Au labda, “Nchi Isiyofaa Kitu.”

Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.

Au “jumba lake mwenyewe la mfalme.”

Au “Milo.” Neno la Kiebrania linalomaanisha “jaza.”

Au “zawadi ya harusi; mahari.”

Au “akaliimarisha.”

Au “Milo.” Neno la Kiebrania linalomaanisha “jaza.”

Au “mafumbo.”

Tnn., “lililofichwa.”

Tnn., “hakubaki na roho yoyote ndani yake.”

Au “maneno.”

Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.

Au “jumba la mfalme.”

Tnn., “kulingana na mkono wa Mfalme Sulemani.”

Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.

Kwa kawaida ilibebwa na wapiga mishale.

Katika Maandiko ya Kiebrania mina moja inalingana na gramu 570. Angalia Nyongeza B14.

Tnn., “waliutafuta uso wa.”

Au “wapanda farasi.”

Au “wapanda farasi.”

Au labda, “kutoka Misri na kutoka Kue; wafanyabiashara wa mfalme waliwanunua kutoka Kue,” huenda ni Kilikia.

Au “Hampaswi kuoana nao.”

Au “wake zake wakawa na uvutano mkubwa kwake.”

Au “waliupotosha.”

Au “haukumtumikia kikamili.”

Hakuwa malkia aliyetawala.

Au labda, “alimwachisha kunyonya.”

Tnn., “alipowaua.”

Tnn., “kuinua mkono wake dhidi ya.”

Au “Milo.” Neno la Kiebrania linalomaanisha “jaza.”

Tnn., “maamuzi yangu.”

Au “ambacho nafsi yako inatamani.”

Au “inayokandamiza.”

Tnn., “mahema yao.”

Tnn., “waliochaguliwa.”

Au “akaliimarisha.”

Au “kuliimarisha.”

Au “alama.”

Au “alama.”

Au “majivu yenye mafuta,” yaani, majivu yaliyojaa mafuta ya dhabihu.

Au “ukapooza.”

Au “alama.”

Au “utulize uso wa.”

Tnn., “Aliujaza mkono wa.”

Au “Utamwambia hivi na hivi.”

Au “sanamu za kuyeyushwa.”

Tnn., “mtu yeyote anayekojoa ukutani.” Huu ni msemo wa Kiebrania wa kuwadharau wanaume.

Angalia Kamusi.

Angalia Kamusi.

Au “jumba la mfalme.”

Tnn., “wakimbiaji.”

Anaitwa pia Abiya.

Au “haukumtumikia kikamili.”

Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.

Yaani, kingono.

Angalia Kamusi.

Au “ulimtumikia kikamili.”

Tnn., “siku zake zote.”

Au “kuimarisha; kujenga upya.”

Au “asiondoke wala kuingia katika eneo la.”

Au “jumba la.”

Au “agano.”

Au “agano lako.”

Au “kuimarisha; kujenga upya.”

Au “kuimarisha; kujenga upya.”

Au “aliyoimarisha; aliyojenga upya.”

Yaani, mwana wa Yeroboamu.

Tnn., “mtu yeyote anayekojoa ukutani.” Huu ni msemo wa Kiebrania wa kuwadharau wanaume.

Au “watu wanaolipiza kisasi chake cha damu.”

Au “jumba la mfalme.”

Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.

Maana yake “Mali ya Ukoo wa Shemeri.”

Tnn., “bwana.”

Au “hekalu la Baali alilojenga.”

Angalia Kamusi.

Maana yake “Mungu Wangu Ni Yehova.”

Tnn., “ninayesimama mbele zake.”

Au “Korongo.”

Au “Korongo.”

Au “makorongo.”

Tnn., “ninayesimama mbele zake.”

Au “unayesababisha Israeli itengwe.”

Angalia Kamusi.

Au “kuchechemea kwa kutumia magongo mawili.”

Au labda, “amesafiri.”

Au “kama manabii.”

Sea moja ilikuwa sawa na lita 7.33 (vibaba 6.66). Angalia Nyongeza B14.

Au “korongo la.”

Au “sitafanya nafsi yako iwe kama nafsi ya.”

Au “nafsi yake.”

Au “iondoe nafsi yangu.”

Au “kuiondoa nafsi yangu.”

Au “kuiondoa nafsi yangu.”

Au “vibanda vyao.”

Au “wilaya za utawala.”

Au “vibanda.”

Au “akawachinja Wasiria wengi.”

Yaani, majira yajayo ya kuchipua.

Tnn., “hesabu.”

Yaani, majira ya kuchipua.

Au “upendo mshikamanifu.”

Au “huenda akaiacha hai nafsi yako.”

Au “iruhusu nafsi yangu iishi.”

Au “kujichagulia mitaa.”

Au “agano hili.”

Inaonekana maneno “wana wa manabii” yanarejelea shule ya kuwafundisha manabii au chama cha manabii.

Au “nafsi yake kwa nafsi yako.”

Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.

Au “nafsi yake kwa nafsi yako.”

Tnn., “Kwa nini roho yako imehuzunika.”

Tnn., “umejiuza.”

Tnn., “mtu yeyote anayekojoa ukutani.” Huu ni msemo wa Kiebrania wa kuwadharau wanaume.

Tnn., “aliyejiuza.”

Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.

Au “utawasukuma.”

Au “malaika.”

Tnn., “kambini.”

Au labda, “mbwa waliramba damu yake mahali ambapo makahaba waliogea.”

Au “jumba la mfalme alilojenga la.”

Angalia Kamusi.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki