KULINGANA NA LUKA
1 Kwa kuwa watu wengi wamejitahidi kukusanya habari kuhusu mambo ambayo tunayasadiki kabisa,+ 2 kama tulivyoyapokea kutoka kwa wale waliokuwa mashahidi wa kujionea tangu mwanzo+ na wahudumu wa ujumbe,+ 3 mheshimiwa Theofilo,+ mimi pia nimefuatilia mambo yote kwa usahihi tangu mwanzo, nami nimeamua kukuandikia mambo hayo kwa utaratibu mzuri, 4 ili ujue kikamili uhakika wa mambo uliyofundishwa kwa mdomo.+
5 Katika siku za Herode,*+ mfalme wa Yudea, kulikuwa na kuhani aliyeitwa Zekaria wa kikundi cha Abiya.+ Mke wake aliitwa Elisabeti na alikuwa wa ukoo wa Haruni. 6 Wote wawili walikuwa waadilifu mbele za Mungu na walitembea bila lawama kulingana na amri na sheria zote za Yehova.* 7 Lakini hawakuwa na mtoto, kwa sababu Elisabeti alikuwa tasa, na wote wawili walikuwa wamezeeka.
8 Alipokuwa akihudumu akiwa kuhani mbele za Mungu wakati wa zamu ya kikundi chake,+ 9 kulingana na desturi ya* ukuhani zamu yake ikafika ya kuingia patakatifu pa Yehova*+ ili kufukiza uvumba.+ 10 Umati wote ulikuwa nje ukisali saa hiyo ya kufukiza uvumba. 11 Malaika wa Yehova* akamtokea, akiwa amesimama upande wa kulia wa madhabahu ya uvumba. 12 Lakini Zekaria alihangaishwa na jambo aliloona, akaogopa sana. 13 Hata hivyo, malaika akamwambia: “Usiogope, Zekaria, kwa sababu dua yako imesikiwa vema, na mke wako Elisabeti atakuzalia mwana, nawe utamwita Yohana.+ 14 Utakuwa na shangwe na furaha nyingi, na wengi watashangilia atakapozaliwa,+ 15 kwa maana atakuwa mkuu mbele za Yehova.*+ Lakini hapaswi kamwe kunywa divai wala kileo,+ naye atajazwa roho takatifu hata kabla ya kuzaliwa,*+ 16 naye atawarudisha wana wengi wa Israeli kwa Yehova* Mungu wao.+ 17 Pia, atamtangulia kwa roho na nguvu za Eliya,+ ili kurudisha mioyo ya akina baba kwa watoto+ na wale wasiotii kwenye hekima ya waadilifu, na kumwandalia Yehova* watu waliotayarishwa.”+
18 Zekaria akamuuliza malaika: “Ninawezaje kuwa na uhakika kuhusu jambo hili? Kwa maana nimezeeka, nao umri wa mke wangu pia umesonga.” 19 Malaika akamjibu: “Mimi ni Gabrieli,+ ninayesimama karibu mbele za Mungu,+ nami nilitumwa nizungumze nawe na kukutangazia habari hii njema. 20 Lakini tazama! utakaa kimya, hutaweza kuongea mpaka siku ambayo mambo hayo yatatendeka, kwa sababu hukuamini maneno yangu ambayo yatatimizwa katika wakati uliowekwa.” 21 Watu wakaendelea kumsubiri Zekaria, nao wakashangaa kwa sababu alikuwa amekawia sana katika patakatifu. 22 Alipotoka hakuweza kuzungumza nao, basi wakajua kwamba alikuwa ameona jambo la kustaajabisha* katika patakatifu. Akaendelea kuwafanyia ishara lakini hakuweza kuongea. 23 Siku zake za utumishi mtakatifu* zilipokwisha, akarudi nyumbani.
24 Baada ya siku chache Elisabeti mke wake akapata mimba, naye hakutoka nyumbani kwa miezi mitano. Alikuwa akisema: 25 “Yehova* amenitendea hivi katika siku hizi. Amenikumbuka ili kuniondolea aibu kati ya watu.”+
26 Katika mwezi wake wa sita, malaika Gabrieli+ akatumwa na Mungu aende katika jiji la Nazareti huko Galilaya, 27 kwa bikira+ aliyeitwa Maria,+ mchumba wa mwanamume aliyeitwa Yosefu wa nyumba ya Daudi. 28 Malaika akaja na kumwambia: “Salamu, wewe uliyebarikiwa sana, Yehova* yuko pamoja nawe.” 29 Lakini Maria akahangaishwa sana na maneno aliyoambiwa, naye akaanza kufikiria maana ya salamu hizo. 30 Basi malaika akamwambia: “Usiogope, Maria, kwa maana umepata kibali cha Mungu. 31 Tazama! utapata mimba* na kuzaa mwana+ nawe utamwita Yesu.+ 32 Huyo atakuwa mkuu+ naye ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi,+ na Yehova* Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake,+ 33 naye atatawala akiwa Mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na Ufalme wake hautakuwa na mwisho.”+
34 Lakini Maria akamuuliza malaika: “Hilo litawezekanaje, kwa kuwa sina uhusiano wa kingono na mwanamume?”+ 35 Malaika akamjibu: “Roho takatifu itakuja juu yako,+ na nguvu za Aliye Juu Zaidi zitakufunika. Kwa hiyo yule atakayezaliwa ataitwa mtakatifu,+ Mwana wa Mungu.+ 36 Tazama! Hata Elisabeti mtu wako wa ukoo, ingawa amezeeka ana mimba ya miezi sita, yule anayejulikana kuwa tasa; 37 kwa sababu kwa Mungu hakuna tangazo* lisilowezekana.”+ 38 Ndipo Maria akasema: “Tazama! Kijakazi wa Yehova!* Na itendeke kwangu kulingana na tangazo lako.” Kisha malaika akaondoka.
39 Basi siku hizo, Maria akafunga safari haraka kwenda kwenye eneo lenye milima, mpaka jiji fulani la Yuda, 40 naye akaingia nyumbani kwa Zekaria na kumsalimu Elisabeti. 41 Elisabeti aliposikia salamu za Maria, mtoto aliyekuwa tumboni mwake akaruka, naye Elisabeti akajazwa roho takatifu 42 na kusema kwa sauti kubwa: “Umebarikiwa kati ya wanawake, na uzao wa tumbo lako umebarikiwa! 43 Imekuwaje nimependelewa hivi kwamba mama ya Bwana wangu amenitembelea? 44 Kwa maana tazama! niliposikia salamu zako, mtoto aliye tumboni mwangu aliruka kwa shangwe. 45 Mwenye furaha pia ni yule aliyeamini, kwa sababu atatimiziwa kikamili mambo aliyoambiwa kutoka kwa Yehova.”*
46 Naye Maria akasema: “Nafsi* yangu inamtukuza Yehova,*+ 47 na roho yangu haitaacha kumshangilia Mungu Mwokozi wangu,+ 48 kwa sababu ametazama hali ya chini ya kijakazi wake.+ Tazama! tangu sasa vizazi vyote vitanitangaza kuwa mwenye furaha,+ 49 kwa sababu Mwenye nguvu amenitendea mambo makuu, nalo jina lake ni takatifu,+ 50 naye huwaonyesha rehema wale wanaomwogopa, kizazi baada ya kizazi.+ 51 Amefanya mambo makuu kwa mkono wake, amewatawanya wenye majivuno katika nia ya mioyo yao.+ 52 Amewashusha watu wenye nguvu kutoka kwenye viti vya ufalme+ na kuwainua watu wa hali ya chini;+ 53 amewashibisha kabisa wenye njaa kwa vitu vyema+ na kuwafukuza mikono mitupu wale waliokuwa na mali. 54 Amekuja kumsaidia Israeli mtumishi wake, amekumbuka rehema zake,+ 55 kama alivyowaahidi mababu zetu, Abrahamu na uzao wake,*+ milele.” 56 Maria akakaa na Elisabeti kwa karibu miezi mitatu, kisha akarudi nyumbani kwake.
57 Wakati wa Elisabeti wa kujifungua ukafika, naye akazaa mtoto wa kiume. 58 Majirani na watu wake wa ukoo wakasikia kwamba Yehova* amemwonyesha rehema nyingi, wakafurahi pamoja naye.+ 59 Siku ya nane wakaja kumtahiri huyo mtoto,+ nao walitaka kumpa jina la baba yake, Zekaria. 60 Lakini mama yake akajibu: “Hapana! ataitwa Yohana.” 61 Wakamwambia: “Hakuna mtu wenu wa ukoo anayeitwa jina hilo.” 62 Kisha wakamuuliza baba yake wakitumia ishara jina alilotaka kumpa. 63 Basi akaomba kibao akaandika: “Yohana ndilo jina lake.”+ Ndipo wote wakashangaa. 64 Mara moja kinywa chake kikafunguliwa na ulimi wake ukawekwa huru, akaanza kuongea,+ akimsifu Mungu. 65 Majirani wao wote wakaogopa, na mambo yote hayo yakaanza kuzungumziwa katika eneo lote la milimani la Yudea. 66 Wote waliosikia mambo hayo wakayaweka moyoni, wakisema: “Mtoto huyu atakuwa mtu wa aina gani?” Kwa maana mkono wa Yehova* ulikuwa pamoja naye.
67 Kisha Zekaria baba yake akajazwa roho takatifu, naye akatoa unabii huu: 68 “Asifiwe Yehova* Mungu wa Israeli,+ kwa sababu amewakumbuka watu wake na kuwaletea ukombozi.+ 69 Naye ametuinulia pembe ya wokovu*+ katika nyumba ya Daudi mtumishi wake,+ 70 kama alivyosema kupitia kinywa cha manabii wake watakatifu tangu zamani,+ 71 kwamba atatuokoa kutoka kwa adui zetu na kutoka mikononi mwa wote wanaotuchukia;+ 72 ili kuonyesha rehema kuhusiana na mababu zetu na kulikumbuka agano lake takatifu,+ 73 kama alivyomwapia Abrahamu babu yetu,+ 74 kwamba atatukomboa kutoka mikononi mwa adui, na kutupatia pendeleo la kumtolea utumishi mtakatifu bila woga 75 kwa ushikamanifu na uadilifu mbele zake siku zetu zote. 76 Lakini wewe, mtoto mchanga, utaitwa nabii wa Aliye Juu Zaidi, kwa maana utaenda mbele za Yehova* ili kutayarisha njia zake,+ 77 kuwapa watu wake ujuzi wa wokovu kupitia kusamehewa dhambi zao,+ 78 kwa sababu ya huruma nyororo za Mungu wetu. Kwa huruma hizo tutapata mapambazuko kutoka juu, 79 ili kuwapa nuru wale wanaokaa gizani na katika kivuli cha kifo+ na kuongoza hatua zetu kwenye njia ya amani.”
80 Yule mtoto akakua na kupata nguvu katika roho, naye aliishi jangwani mpaka siku aliyojionyesha waziwazi kwa Israeli.
2 Basi katika siku hizo Kaisari Augusto alitoa amri kwamba watu wote wa dunia inayokaliwa waandikishwe. 2 (Uandikishaji huo wa kwanza ulifanyika Kirenio alipokuwa gavana wa Siria.) 3 Na watu wote wakaenda kuandikishwa kila mmoja katika jiji lake. 4 Yosefu+ pia akatoka jiji la Nazareti huko Galilaya akapanda kwenda Yudea katika jiji la Daudi, linaloitwa Bethlehemu,+ kwa sababu alikuwa wa nyumba na familia ya Daudi. 5 Alienda kuandikishwa pamoja na Maria ambaye alikuwa amemwoa kama ilivyoahidiwa,+ naye alikuwa karibu kuzaa.+ 6 Wakiwa huko, wakati wake wa kuzaa ukafika. 7 Naye akamzaa mwana, mzaliwa wake wa kwanza,+ akamfunga kwa vitambaa na kumlaza katika hori,+ kwa sababu hawakupata nafasi katika nyumba za wageni.
8 Kulikuwa pia na wachungaji katika eneo hilo ambao waliishi nje wakichunga makundi yao usiku. 9 Ghafla malaika wa Yehova* akawatokea, na utukufu wa Yehova* ukawaangazia pande zote, nao wakaogopa sana. 10 Lakini malaika akawaambia: “Msiogope, kwa maana tazama! ninawatangazia habari njema ya shangwe kubwa ambayo watu wote watakuwa nayo. 11 Kwa sababu leo katika jiji la Daudi,+ amezaliwa mwokozi+ ambaye ni Kristo, Bwana.+ 12 Na hii ndiyo ishara kwenu: Mtamkuta mtoto aliyefungwa kwa vitambaa akiwa amelala katika hori.” 13 Ghafla wakaona umati wa jeshi la mbinguni ukiwa pamoja na yule malaika,+ wakimsifu Mungu wakisema: 14 “Utukufu kwa Mungu katika vilele vilivyo juu, na amani duniani kwa watu wenye nia njema.”*
15 Baada ya malaika kurudi mbinguni, wachungaji wakaanza kuambiana: “Twendeni Bethlehemu tukaone jambo hili ambalo Yehova* ametujulisha.” 16 Wakaenda haraka wakamkuta Maria na Yosefu, na yule mtoto mchanga akiwa amelala katika hori. 17 Walipoona jambo hilo, wakawaeleza ujumbe walioambiwa kuhusu mtoto huyo mchanga. 18 Wote waliosikia wakashangazwa na mambo waliyoambiwa na wachungaji, 19 lakini Maria akaanza kuyahifadhi maneno hayo yote, na kukata kauli moyoni mwake.+ 20 Basi wachungaji wakarudi, wakimtukuza na kumsifu Mungu kwa sababu ya mambo yote waliyosikia na kuona, kama tu walivyokuwa wameambiwa.
21 Baada ya siku nane, wakati ulipofika wa kumtahiri,+ wakampa jina Yesu, jina alilopewa na malaika kabla ya Maria kupata mimba.+
22 Pia, wakati ulipofika wa kuwatakasa kulingana na Sheria ya Musa,+ wakamleta Yerusalemu ili kumtoa kwa Yehova,* 23 kama ilivyoandikwa katika Sheria ya Yehova:* “Kila mzaliwa wa kwanza* wa kiume lazima ataitwa mtakatifu kwa Yehova.”*+ 24 Wakatoa dhabihu kama ilivyoandikwa katika Sheria ya Yehova:* “njiwa tetere wawili au hua wawili wachanga.”+
25 Na tazama! kulikuwa na mtu fulani Yerusalemu aliyeitwa Simeoni, alikuwa mwadilifu na alimwogopa Mungu, naye alikuwa akisubiri faraja ya Israeli,+ na roho takatifu ilikuwa juu yake. 26 Zaidi ya hayo, Mungu alikuwa amemfunulia kupitia roho takatifu kwamba hangekufa kabla ya kumwona Kristo wa Yehova.* 27 Akaja hekaluni akiongozwa na roho, na wazazi wa yule mtoto Yesu walipomleta ili kufanya kulingana na desturi ya Sheria,+ 28 akambeba yule mtoto mikononi mwake akamsifu Mungu akisema: 29 “Sasa, Bwana Mwenye Enzi Kuu, unaruhusu mtumwa wako aende kwa amani+ kulingana na tangazo lako, 30 kwa sababu macho yangu yameona njia yako ya kuleta wokovu+ 31 ambayo umetayarisha machoni pa watu wote,+ 32 nuru+ ya kuondoa kitambaa* kwa mataifa+ na utukufu wa watu wako Israeli.” 33 Baba na mama ya yule mtoto wakaendelea kushangazwa na mambo yaliyokuwa yakisemwa kumhusu. 34 Pia, Simeoni akawabariki na kumwambia Maria, mama ya yule mtoto: “Tazama! Mtoto huyu amewekwa rasmi kwa ajili ya kuanguka+ na kuinuka tena kwa wengi katika Israeli+ na kuwa ishara itakayosemwa vibaya+ 35 (ndiyo, upanga mrefu utakuchoma*),+ ili mawazo ya mioyo mingi yafunuliwe.”
36 Kulikuwa na nabii wa kike aliyeitwa Ana, binti ya Fanueli, wa kabila la Asheri, ambaye alikuwa amezeeka. Alikuwa ameishi na mume wake kwa miaka saba baada ya kuolewa,* 37 na sasa alikuwa mjane mwenye umri wa miaka 84. Hakukosa kamwe hekaluni, akitoa utumishi mtakatifu usiku na mchana, akifunga na kutoa dua. 38 Wakati huohuo, akaja na kuanza kumshukuru Mungu akiwaambia kuhusu mtoto huyo wale wote waliokuwa wakisubiri ukombozi wa Yerusalemu.+
39 Basi, baada ya kufanya mambo yote kulingana na Sheria ya Yehova,*+ wakarudi huko Galilaya kwenye jiji la kwao la Nazareti.+ 40 Yule mtoto akaendelea kukua na kupata nguvu, akazidi kuwa na hekima, na akaendelea kuwa na kibali cha Mungu.+
41 Wazazi wake walikuwa na desturi ya kwenda Yerusalemu kila mwaka kwa ajili ya sherehe ya Pasaka.+ 42 Na alipokuwa na umri wa miaka 12, wakapanda kwenda kulingana na desturi ya sherehe.+ 43 Siku za sherehe zilipokwisha wakaanza kurudi nyumbani, lakini mvulana Yesu akabaki Yerusalemu, hata hivyo, wazazi wake hawakujua. 44 Walisafiri umbali wa siku moja wakidhani Yesu alikuwa miongoni mwa wasafiri, kisha wakaanza kumtafuta kati ya watu wao wa ukoo na watu waliowafahamu. 45 Walipomkosa wakarudi mpaka Yerusalemu na kumtafuta kwa bidii. 46 Baada ya siku tatu wakampata hekaluni akiwa ameketi katikati ya walimu akiwasikiliza na kuwauliza maswali. 47 Lakini wote waliomsikiliza walikuwa wakishangazwa na majibu yake na uwezo wake wa kuelewa.+ 48 Wazazi wake walipomwona wakashangaa, mama yake akamwambia: “Mwanangu, kwa nini umetutendea hivi? Mimi na baba yako tumekuwa tukikutafuta tukiwa na wasiwasi mwingi.” 49 Lakini akawaambia: “Kwa nini mlikuwa mkinitafuta? Je, hamkujua kwamba ninapaswa kuwa katika nyumba ya Baba yangu?”+ 50 Hata hivyo, hawakuelewa mambo aliyokuwa akiwaambia.
51 Yesu akashuka pamoja nao kurudi Nazareti, akaendelea kuwatii.*+ Naye mama yake akayahifadhi kwa uangalifu mambo hayo yote moyoni mwake.+ 52 Yesu akaendelea kukua na kupata hekima zaidi, pia akazidi kupata kibali cha Mungu na wanadamu.
3 Katika mwaka wa 15 wa utawala wa Kaisari Tiberio, Pontio Pilato alipokuwa gavana wa Yudea, Herode*+ alipokuwa mtawala wa wilaya * ya Galilaya, Filipo ndugu yake alipokuwa mtawala wa wilaya ya Iturea na Trakoniti, naye Lisania alipokuwa mtawala wa wilaya ya Abilene, 2 katika siku za Kayafa+ na mkuu wa makuhani Anasi, Yohana+ mwana wa Zekaria akiwa nyikani, alipokea ujumbe kutoka kwa Mungu.+
3 Basi akaenda katika maeneo yote yaliyokuwa karibu na Yordani, akiwahubiria watu wabatizwe ili kuonyesha kwamba wametubu na hivyo wasamehewe dhambi zao,+ 4 kama ilivyoandikwa katika kitabu cha maneno ya nabii Isaya: “Kuna mtu anayepaza sauti nyikani: ‘Tayarisheni njia ya Yehova!* Nyoosheni barabara zake.+ 5 Lazima kila bonde lijazwe, na kila mlima na kilima visawazishwe; lazima barabara zilizopinda zinyooshwe, na barabara zenye miparuzo zilainishwe; 6 na wote wenye mwili* wataona wokovu wa Mungu.’”*+
7 Basi akaanza kuuambia umati uliokuja kwake ili awabatize: “Enyi uzao wa nyoka,* ni nani amewaonya mkimbie ghadhabu inayokuja?+ 8 Basi zaeni matunda yanayoonyesha toba. Wala msijiambie, ‘Abrahamu ndiye baba yetu.’ Kwa maana ninawaambia, Mungu anaweza kumwinulia Abrahamu watoto kutoka kwenye mawe haya. 9 Kwa kweli, tayari shoka limewekwa kwenye mzizi wa miti. Basi, kila mti usiozaa matunda mazuri utakatwa na kutupwa motoni.”+
10 Umati ulikuwa ukimuuliza: “Basi, tufanye nini?” 11 Akawajibu: “Mtu aliye na mavazi mawili* ampe vazi moja yule ambaye hana, na aliye na chakula afanye vivyo hivyo.”+ 12 Hata wakusanya kodi wakaja ili wabatizwe,+ wakamuuliza: “Mwalimu, tufanye nini?” 13 Akawaambia: “Msidai* zaidi ya kiwango kilichowekwa cha kodi.”+ 14 Pia, wale walio katika utumishi wa jeshi walikuwa wakimuuliza: “Tufanye nini?” Akawaambia: “Msimsumbue* mtu yeyote wala kumshtaki mtu yeyote kwa uwongo,+ bali mtosheke na posho yenu.”*
15 Kwa kuwa watu walikuwa wakitarajia, wote walikuwa wakijiuliza moyoni mwao kuhusu Yohana, “Je, labda huyu ndiye Kristo?”+ 16 Yohana akawajibu: “Mimi ninawabatiza kwa maji, lakini anakuja mwenye nguvu kuliko mimi, ambaye sistahili kufungua kamba za viatu vyake.+ Yeye atawabatiza kwa roho takatifu na moto.+ 17 Sepetu yake ya kupepetea imo mkononi mwake ili kuusafisha kabisa uwanja wake wa kupuria, na kukusanya ngano katika ghala lake, lakini atayateketeza makapi kwa moto usioweza kuzimwa.”
18 Pia, aliwahimiza kwa maneno mengine mengi na akaendelea kuwatangazia watu habari njema. 19 Yohana alikuwa amemkaripia Herode mtawala wa wilaya kwa kumchukua Herodia mke wa ndugu yake na kwa sababu ya matendo yote maovu ambayo Herode alikuwa amefanya, 20 aliongeza hili pia kwenye matendo hayo yote: Alimfunga Yohana gerezani.+
21 Baada ya watu wote kubatizwa, Yesu pia akabatizwa.+ Alipokuwa akisali, mbingu zikafunguka,+ 22 roho takatifu ikashuka juu yake ikiwa na umbo kama la njiwa, na sauti ikasikika kutoka mbinguni ikisema: “Wewe ni Mwanangu, mpendwa; nimekukubali.”+
23 Yesu+ alikuwa na umri wa miaka 30 hivi alipoanza kazi yake,+ akiwa mwana, kama alivyoonwa,
wa Yosefu,+
mwana wa Heli,
24 mwana wa Mathati,
mwana wa Lawi,
mwana wa Melki,
mwana wa Yanai,
mwana wa Yosefu,
25 mwana wa Matathia,
mwana wa Amosi,
mwana wa Nahumu,
mwana wa Esli,
mwana wa Nagai,
26 mwana wa Maathi,
mwana wa Matathia,
mwana wa Semei,
mwana wa Yoseki,
mwana wa Yoda,
27 mwana wa Yoanani,
mwana wa Resa,
mwana wa Zerubabeli,+
mwana wa Shealtieli,+
mwana wa Neri,
28 mwana wa Melki,
mwana wa Adi,
mwana wa Kosamu,
mwana wa Elmadamu,
mwana wa Eri,
29 mwana wa Yesu,
mwana wa Eliezeri,
mwana wa Yorimu,
mwana wa Mathati,
mwana wa Lawi,
30 mwana wa Simioni,
mwana wa Yuda,
mwana wa Yosefu,
mwana wa Yonamu,
mwana wa Eliakimu,
31 mwana wa Melea,
mwana wa Mena,
mwana wa Matatha,
mwana wa Nathani,+
mwana wa Daudi,+
mwana wa Obedi,+
mwana wa Boazi,+
mwana wa Salmoni,+
mwana wa Nashoni,+
33 mwana wa Aminadabu,
mwana wa Arni,
mwana wa Hezroni,
mwana wa Perezi,+
mwana wa Yuda,+
mwana wa Isaka,+
mwana wa Abrahamu,+
mwana wa Tera,+
mwana wa Nahori,+
mwana wa Reu,+
mwana wa Pelegi,+
mwana wa Eberi,+
mwana wa Shela,+
36 mwana wa Kainani,
mwana wa Arpakshadi,+
mwana wa Shemu,+
mwana wa Noa,+
mwana wa Lameki,+
mwana wa Enoko,
mwana wa Yaredi,+
mwana wa Mahalaleeli,+
mwana wa Kainani,+
mwana wa Sethi,+
mwana wa Adamu,+
mwana wa Mungu.
4 Basi Yesu, akiwa amejaa roho takatifu, akaondoka Yordani, naye akaongozwa na roho kwenda nyikani+ 2 kwa siku 40, akijaribiwa na Ibilisi.+ Kipindi hicho chote hakula chakula, basi muda huo ulipokwisha, akahisi njaa. 3 Ndipo Ibilisi akamwambia: “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, liambie jiwe hili liwe mkate.” 4 Lakini Yesu akamjibu: “Imeandikwa, ‘Mwanadamu hataishi kwa mkate tu.’”+
5 Basi akampeleka juu na kumwonyesha mara moja falme zote za dunia inayokaliwa.+ 6 Kisha Ibilisi akamwambia: “Nitakupa mamlaka yote hii na utukufu wake, kwa sababu nimepewa,+ nami humpa yeyote ninayetaka. 7 Kwa hiyo, ukifanya tendo la ibada mbele yangu, yote itakuwa yako.” 8 Yesu akamjibu: “Imeandikwa, ‘Yehova* Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.’”+
9 Kisha akampeleka Yerusalemu, akamsimamisha juu ya mnara wa* hekalu na kumwambia: “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, jitupe chini kutoka hapa,+ 10 kwa maana imeandikwa, ‘Atawaagiza malaika zake kukuhusu wewe, ili wakulinde,’ 11 nao, ‘Watakubeba mikononi mwao, ili mguu wako usigonge jiwe.’”+ 12 Yesu akamjibu: “Imesemwa, ‘Usimjaribu Yehova* Mungu wako.’”+ 13 Kwa hiyo Ibilisi, alipomaliza majaribu yote, akamwacha mpaka wakati mwingine unaofaa.+
14 Basi Yesu akarudi Galilaya+ katika nguvu za roho. Na habari nzuri kumhusu zikaenea katika maeneo yote yaliyo karibu. 15 Pia, akaanza kufundisha katika masinagogi yao, naye akaheshimiwa na watu wote.
16 Kisha akaenda Nazareti,+ mahali alipolelewa, na kulingana na desturi yake siku ya Sabato, akaingia katika sinagogi+ naye akasimama ili kusoma. 17 Basi akapewa kitabu cha kukunjwa cha nabii Isaya, akakifungua na kupata mahali palipoandikwa: 18 “Roho ya Yehova* iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta ili niwatangazie maskini habari njema. Alinituma niwatangazie mateka uhuru na vipofu kuona tena, kuwaweka huru waliopondeka,+ 19 kuhubiri mwaka wa Yehova* unaokubalika.”+ 20 Ndipo akakikunja kitabu hicho na kumrudishia mtumishi, kisha akaketi; na wote katika sinagogi walikuwa wakimtazama kwa makini. 21 Akaanza kuwaambia: “Leo andiko hili ambalo mmetoka kusikia limetimia.”+
22 Wote wakaanza kutoa ushahidi unaofaa kumhusu na kushangazwa na maneno yenye neema yaliyokuwa yakitoka kinywani mwake,+ nao wakawa wakiambiana: “Huyu ni mwana wa Yosefu, sivyo?”+ 23 Ndipo akawaambia: “Bila shaka mtautumia mfano huu kwangu, ‘Daktari, jiponye mwenyewe. Fanya pia katika eneo la nyumbani kwenu mambo tuliyosikia yamefanywa huko Kapernaumu.’”+ 24 Basi akawaambia: “Kwa kweli ninawaambia hakuna nabii anayekubaliwa katika eneo la nyumbani kwao.+ 25 Kwa mfano, kwa kweli ninawaambia: Kulikuwa na wajane wengi Israeli siku za Eliya, mbingu zilipofungwa kwa miaka mitatu na miezi sita, kukawa na njaa kubwa katika nchi yote.+ 26 Lakini Eliya hakutumwa kwa yeyote kati ya wanawake hao, bali kwa mjane mmoja huko Sarefathi katika nchi ya Sidoni.+ 27 Pia, kulikuwa na wenye ukoma wengi Israeli siku za nabii Elisha; lakini hakuna hata mmoja wao aliyetakaswa,* ila Naamani Msiria.”+ 28 Ndipo wote katika sinagogi waliokuwa wakisikia mambo hayo wakajawa na hasira,+ 29 wakasimama na kumtoa haraka nje ya jiji mpaka kwenye ukingo wa mlima ambao jiji lao lilikuwa limejengwa, ili wamtupe chini. 30 Lakini akapita katikati yao na kwenda zake.+
31 Kisha akashuka kwenda jiji la Kapernaumu, huko Galilaya. Naye alikuwa akiwafundisha siku ya Sabato,+ 32 nao wakashangazwa na njia yake ya kufundisha,+ kwa sababu alikuwa akizungumza kwa mamlaka. 33 Basi katika sinagogi kulikuwa na mtu mwenye roho mwovu, naye akapiga kelele akisema:+ 34 “Ah! Kwa nini unatusumbua, wewe Yesu Mnazareti?+ Je, umekuja kutuangamiza? Ninajua wewe ni nani, Mtakatifu wa Mungu.”+ 35 Lakini Yesu akamkemea, akisema: “Nyamaza na umtoke.” Basi baada ya kumwangusha mtu huyo mbele yao, yule roho mwovu akamtoka bila kumuumiza. 36 Wote wakashangaa na kuanza kuambiana: “Anazungumza kwa mamlaka sana! Anawaagiza roho waovu kwa mamlaka na nguvu, nao wanatoka!” 37 Basi habari kumhusu zikazidi kuenea kila mahali katika maeneo yaliyokuwa karibu.
38 Alipotoka katika sinagogi akaenda nyumbani kwa Simoni. Mama mkwe wa Simoni alikuwa na homa kali, wakamwomba Yesu amponye.+ 39 Yesu akasimama kando yake, akaikemea ile homa, ikaisha. Papo hapo akasimama na kuanza kuwahudumia.
40 Jua lilipokuwa likitua, wote waliokuwa na watu wenye magonjwa mbalimbali wakawaleta kwake. Akawaponya kwa kuweka mikono yake juu ya kila mgonjwa.+ 41 Roho waovu pia wakawatoka watu wengi, wakipaza sauti na kusema: “Wewe ndiye Mwana wa Mungu.”+ Lakini aliwakemea na hakuwaruhusu waseme,+ kwa maana walijua yeye ni Kristo.+
42 Hata hivyo, kulipopambazuka, akaenda mahali pasipo na watu.+ Lakini umati ukaanza kumtafuta* na walipofika mahali alipokuwa, wakajaribu kumzuia asiondoke. 43 Lakini akawaambia: “Ni lazima pia nitangaze habari njema ya Ufalme wa Mungu katika majiji mengine, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.”+ 44 Basi akaendelea kuhubiri katika masinagogi ya Yudea.
5 Pindi moja, Yesu alikuwa amesimama kando ya ziwa la Genesareti*+ na umati ulikuwa umemsonga ili kusikiliza neno la Mungu. 2 Akaona mashua mbili zikiwa zimeegeshwa kando ya ziwa, lakini wavuvi walikuwa wametoka na walikuwa wakiosha nyavu zao.+ 3 Akaingia katika mashua moja iliyokuwa ya Simoni, akamwomba aivute mbali kidogo na nchi kavu. Kisha akaketi na kuanza kuwafundisha watu akiwa kwenye mashua. 4 Alipoacha kuzungumza, akamwambia Simoni: “Peleka mashua mahali penye kina, kisha mshushe nyavu zenu, mvue samaki.” 5 Simoni akamjibu: “Mwalimu, tumejitahidi kuvua samaki usiku wote na hatukupata chochote,+ lakini nitazishusha nyavu kama ulivyoniagiza.” 6 Basi walipofanya hivyo, wakavua* samaki wengi sana hivi kwamba nyavu zao zikaanza kukatika.+ 7 Wakawaita wenzao waliokuwa katika ile mashua nyingine waje kuwasaidia, wakaja na kujaza mashua zote mbili, nazo zikaanza kuzama. 8 Simoni Petro alipoona hivyo, akaanguka magotini pa Yesu na kusema: “Bwana ondoka kwangu, kwa sababu mimi ni mtu mwenye dhambi.” 9 Kwa maana yeye na wenzake walishangazwa sana na samaki wengi waliovua. 10 Pia, Yakobo na Yohana, wana wa Zebedayo,+ ambao walishirikiana na Simoni wakashangaa. Lakini Yesu akamwambia Simoni: “Acha kuogopa. Kuanzia sasa utakuwa ukiwavua watu wakiwa hai.”+ 11 Basi wakazirudisha mashua kwenye nchi kavu, wakaacha kila kitu na kumfuata.+
12 Pindi nyingine alipokuwa katika jiji fulani, tazama! kulikuwa na mwanamume aliyejaa ukoma! Alipomwona Yesu, akajiangusha kifudifudi na kumwomba: “Bwana, ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.”+ 13 Basi Yesu akanyoosha mkono wake akamgusa na kusema: “Ninataka! Takasika.” Mara moja ule ukoma ukaisha.+ 14 Kisha akamwagiza mtu huyo asimwambie mtu yeyote: “Bali nenda ukajionyeshe kwa kuhani, kisha utoe toleo la kutakaswa kwako, kama alivyoagiza Musa,+ ili kuwa ushahidi kwao.”+ 15 Lakini habari kumhusu zikazidi kuenea, na umati mkubwa ulikuwa ukikusanyika ili kumsikiliza na kuponywa magonjwa yao.+ 16 Hata hivyo, mara kwa mara alienda mahali pasipo na watu ili kusali.
17 Siku moja alipokuwa akifundisha, Mafarisayo na walimu wa sheria kutoka kila kijiji cha Galilaya na Yudea na kutoka Yerusalemu walikuwa wameketi hapo; na Yehova* alikuwa amempa nguvu za kuponya.+ 18 Na tazama! kulikuwa na wanaume waliombeba kwenye kitanda* mtu aliyepooza, nao wakajaribu kumwingiza ndani na kumweka mbele ya Yesu.+ 19 Waliposhindwa kumwingiza kwa sababu ya umati, wakapanda kwenye paa, wakaondoa vigae na kumshusha akiwa kwenye kitanda kati ya wale waliokuwa mbele ya Yesu. 20 Alipoona imani yao, akamwambia yule mtu: “Ewe mtu, umesamehewa dhambi zako.”+ 21 Ndipo waandishi na Mafarisayo wakaanza kujadiliana: “Huyu ni nani anayesema makufuru? Ni nani anayeweza kusamehe dhambi isipokuwa Mungu peke yake?”+ 22 Lakini Yesu, akifahamu mawazo yao akawauliza: “Mnawaza nini katika mioyo yenu? 23 Ni jambo gani rahisi zaidi kusema, ‘Umesamehewa dhambi zako,’ au kusema, ‘Simama utembee’? 24 Lakini ili mjue kwamba Mwana wa binadamu ana mamlaka ya kusamehe dhambi duniani—” akamwambia yule mtu aliyepooza: “Ninakuambia, Simama, uchukue kitanda chako, uende nyumbani.”+ 25 Ndipo akasimama mbele yao, akachukua kitanda chake, akaenda nyumbani, akimtukuza Mungu. 26 Kisha wote wakashangaa wakaanza kumtukuza Mungu, wakastaajabu na kusema: “Leo tumeona mambo ya ajabu!”
27 Baada ya mambo hayo akaenda nje na kumwona mkusanya kodi anayeitwa Lawi akiwa ameketi kwenye ofisi ya kodi, akamwambia: “Njoo uwe mfuasi wangu.”+ 28 Naye akasimama, akaacha kila kitu na kuanza kumfuata. 29 Kisha Lawi akamwandalia Yesu karamu kubwa nyumbani kwake, na kulikuwa na umati mkubwa wa wakusanya kodi na wengine waliokuwa wakila* pamoja nao.+ 30 Ndipo Mafarisayo na waandishi wao wakaanza kuwalalamikia wanafunzi wake, wakisema: “Kwa nini mnakula na kunywa pamoja na wakusanya kodi na watenda dhambi?”+ 31 Yesu akawajibu: “Watu wenye afya hawahitaji daktari, lakini wagonjwa wanamhitaji.+ 32 Sikuja kuwaita waadilifu, bali kuwahimiza watenda dhambi watubu.”+
33 Wakamwambia: “Wanafunzi wa Yohana hufunga mara nyingi na kutoa dua, na pia wanafunzi wa Mafarisayo, lakini wanafunzi wako hula na kunywa.”+ 34 Yesu akawaambia: “Hamwezi kuwafanya rafiki za bwana harusi wafunge bwana harusi akiwa pamoja nao, sivyo? 35 Lakini siku zitakuja ambapo kwa kweli bwana harusi+ ataondolewa kwao; ndipo watakapofunga siku hizo.”+
36 Pia, akawapa mfano: “Hakuna mtu anayekata kiraka cha vazi jipya la nje na kukishona kwenye vazi la zamani. Akifanya hivyo, kiraka kipya hurarua vazi la zamani na kiraka kipya hakilingani na vazi la zamani.+ 37 Pia, hakuna mtu anayeweka divai mpya katika viriba vya divai vilivyochakaa. Akifanya hivyo, divai mpya itavipasua viriba, nayo itamwagika na viriba vitaharibika. 38 Lakini divai mpya lazima iwekwe katika viriba vipya vya divai. 39 Mtu anapokunywa divai ya zamani hapendi divai mpya, kwa maana husema, ‘Ile ya zamani ndiyo nzuri.’”
6 Siku moja ya Sabato Yesu alipokuwa akipita katika mashamba ya nafaka, wanafunzi wake walikuwa wakivunja na kula masuke ya nafaka, + wakiyapukusa kwa mikono yao.+ 2 Ndipo baadhi ya Mafarisayo wakauliza: “Kwa nini mnafanya jambo lisilo halali siku ya Sabato?”+ 3 Lakini Yesu akawajibu: “Je, hamjasoma alilofanya Daudi wakati yeye na wanaume waliokuwa pamoja naye walipohisi njaa?+ 4 Jinsi alivyoingia katika nyumba ya Mungu akapokea mikate ya toleo,* akala na pia akawapa wanaume waliokuwa pamoja naye, mikate ambayo si halali kwa yeyote kula ila makuhani tu?”+ 5 Kisha akawaambia: “Mwana wa binadamu ndiye Bwana wa Sabato.”+
6 Siku nyingine ya Sabato+ aliingia katika sinagogi, akaanza kufundisha. Kulikuwa na mtu aliyepooza mkono wa kulia.+ 7 Waandishi na Mafarisayo walikuwa wakimwangalia Yesu kwa makini ili waone kama angeponya katika siku ya Sabato, ili wapate sababu ya kumshtaki. 8 Hata hivyo, alijua mawazo yao,+ basi akamwambia yule mtu aliyepooza mkono: “Inuka usimame hapa katikati.” Naye akainuka na kusimama hapo. 9 Kisha Yesu akawauliza: “Je, ni halali kufanya mema au kufanya mabaya siku ya Sabato, kuokoa uhai* au kuuangamiza?”+ 10 Baada ya kuwatazama wote waliokuwapo, Yesu akamwambia mtu huyo: “Nyoosha mkono wako.” Akaunyoosha, nao ukapona. 11 Lakini wakakasirika sana, wakaanza kushauriana kuhusu jambo ambalo wangemtendea Yesu.
12 Siku moja, Yesu alienda mlimani kusali,+ naye akasali kwa Mungu usiku wote.+ 13 Kulipokucha akawaita wanafunzi wake na kuchagua 12 kati yao, ambao pia aliwaita mitume:+ 14 Simoni, ambaye pia alimwita jina Petro, Andrea ndugu yake, Yakobo, Yohana, Filipo,+ Bartholomayo, 15 Mathayo, Tomasi,+ Yakobo mwana wa Alfayo, Simoni anayeitwa “mwenye bidii,” 16 Yuda mwana wa Yakobo, na Yuda Iskariote, aliyegeuka kuwa msaliti.
17 Yesu akashuka pamoja nao akasimama mahali tambarare, na kulikuwa na umati mkubwa wa wanafunzi wake, na umati mkubwa wa watu kutoka Yudea yote na Yerusalemu na eneo la pwani la Tiro na Sidoni, waliokuja kumsikiliza na kuponywa magonjwa. 18 Hata aliwaponya wale waliosumbuliwa na roho waovu. 19 Umati wote ulikuwa ukijaribu kumgusa, kwa sababu nguvu zilikuwa zikimtoka+ na kuwaponya wote.
20 Akainua macho na kuwatazama wanafunzi wake na kusema:
“Wenye furaha ni ninyi maskini, kwa sababu Ufalme wa Mungu ni wenu.+
21 “Wenye furaha ni ninyi mlio na njaa sasa, kwa sababu mtashiba.+
“Wenye furaha ni ninyi mnaolia sasa, kwa sababu mtacheka.+
22 “Wenye furaha ni ninyi watu wanapowachukia,+ wanapowatenga,+ wanapowashutumu, na kuwachafulia jina* kwa ajili ya Mwana wa binadamu. 23 Siku hiyo shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa maana tazama! thawabu yenu ni kubwa mbinguni, kwa kuwa mababu zao waliwatendea manabii mambo hayohayo.+
24 “Lakini ole wenu ninyi matajiri,+ kwa sababu mnapata faraja yenu kikamili.+
25 “Ole wenu ninyi mlioshiba sasa, kwa sababu mtakuwa na njaa.
“Ole wenu ninyi mnaocheka sasa, kwa sababu mtaomboleza na kulia.+
26 “Ole wenu watu wote wanapowasifu,+ kwa maana hivyo ndivyo mababu zao walivyowatendea manabii wa uwongo.
27 “Lakini ninawaambia ninyi mnaosikiliza: Endeleeni kuwapenda adui zenu na kuwatendea mema wale wanaowachukia,+ 28 kuwabariki wale wanaowalaani, na kusali kwa ajili ya wale wanaowatukana.+ 29 Anayekupiga kwenye shavu moja, mgeuzie pia shavu lingine; na anayechukua vazi lako la nje, usimzuilie hata vazi la ndani.+ 30 Mpe kila mtu anayekuomba,+ na yule anayechukua vitu vyako, usimwombe akurudishie.
31 “Pia, kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.+
32 “Mkiwapenda wale wanaowapenda, mnapata faida gani? Kwa maana hata watenda dhambi huwapenda wale wanaowapenda.+ 33 Na mkiwatendea mema wale wanaowatendea mema, mnapata faida gani? Hata watenda dhambi hufanya vivyo hivyo. 34 Pia, mkiwakopesha* wale tu ambao mnatumaini watawalipa, mnapata faida gani?+ Hata watenda dhambi huwakopesha watenda dhambi ili warudishiwe kiasi kilekile. 35 Badala yake, endeleeni kuwapenda adui zenu, kutenda mema, na kukopesha bila kutumaini kurudishiwa;+ nanyi mtapata thawabu kubwa, na mtakuwa wana wa Aliye Juu Zaidi, kwa sababu yeye huwaonyesha fadhili hata watu wasio na shukrani na waovu.+ 36 Endeleeni kuwa wenye rehema, kama Baba yenu alivyo mwenye rehema.+
37 “Zaidi ya hayo, acheni kuhukumu, nanyi hamtahukumiwa kamwe;+ na acheni kulaumu, nanyi hamtalaumiwa kamwe. Endeleeni kusamehe,* nanyi mtasamehewa.*+ 38 Muwe na mazoea ya kuwapa watu, nanyi mtapewa.+ Watawamwagia kwenye mfuko wa nguo zenu kipimo kizuri, kilichoshindiliwa, kilichotikiswa, na kufurika. Kwa maana kwa kipimo mnachowapimia watu, ndicho watakachowapimia.”
39 Kisha akawaambia mfano huu: “Je, kipofu anaweza kumwongoza kipofu mwenzake? Wote watatumbukia shimoni, sivyo?+ 40 Mwanafunzi hampiti mwalimu wake, lakini kila mtu aliyefundishwa kikamili atakuwa kama mwalimu wake. 41 Basi, kwa nini unautazama unyasi ulio katika jicho la ndugu yako lakini hutambui boriti lililo katika jicho lako mwenyewe?+ 42 Unawezaje kumwambia ndugu yako, ‘Ndugu, niruhusu niutoe unyasi ulio katika jicho lako,’ wakati wewe mwenyewe huoni boriti lililo katika jicho lako? Mnafiki! Kwanza toa boriti katika jicho lako, kisha utaona vizuri jinsi ya kuutoa unyasi ulio katika jicho la ndugu yako.
43 “Kwa maana hakuna mti mzuri unaozaa matunda yaliyooza, wala hakuna mti uliooza unaozaa matunda mazuri.+ 44 Kwa maana kila mti hujulikana kwa matunda yake.+ Kwa mfano, watu hawachumi tini kwenye miiba, wala kukata zabibu kwenye miti ya miiba. 45 Mtu mwema hutoa mambo mema kwenye hazina njema ya moyo wake, lakini mtu mwovu hutoa maovu kwenye hazina yake mbovu; kwa maana kinywa husema mambo yaliyojaa moyoni.+
46 “Basi kwa nini mnaniita ‘Bwana! Bwana!’ lakini hamfanyi mambo ninayosema?+ 47 Nitawaonyesha jinsi alivyo kila mtu anayekuja kwangu na kusikia maneno yangu na kisha kuyatenda:+ 48 Ni kama mtu aliyejenga nyumba kwa kuchimba kina kirefu na kuweka msingi kwenye mwamba. Baadaye, mafuriko yalipotokea, mto ukaipiga nyumba hiyo, lakini haikutikisika, kwa sababu ilikuwa imejengwa vizuri.+ 49 Kwa upande mwingine, yule anayesikia na hatendi,+ ni kama mtu aliyejenga nyumba juu ya udongo, bila msingi. Mto ukaipiga nyumba hiyo, nayo ikaporomoka mara moja, na kuharibika kabisa.”
7 Alipomaliza kuzungumza na watu, akaingia Kapernaumu. 2 Ofisa fulani wa jeshi alikuwa na mtumwa aliyempenda sana, na ambaye alikuwa mgonjwa sana karibu kufa.+ 3 Aliposikia kuhusu Yesu, akawatuma wazee fulani wa Wayahudi wamwombe Yesu aje kumponya mtumwa wake. 4 Walipofika kwa Yesu wakamsihi sana wakisema: “Mfanyie jambo hilo, anastahili 5 kwa maana analipenda taifa letu na yeye ndiye aliyetujengea sinagogi.” 6 Basi Yesu akaenda pamoja nao. Alipokaribia nyumba hiyo, yule ofisa wa jeshi alikuwa tayari amewatuma rafiki zake wamwambie: “Bwana, usijisumbue, kwa maana mimi sistahili uingie ndani ya nyumba yangu.+ 7 Ndiyo sababu niliona sistahili kuja kwako. Lakini sema tu neno, na mtumishi wangu atapona. 8 Kwa maana mimi pia niko chini ya mamlaka, na nina wanajeshi walio chini yangu, nami humwambia mmoja, ‘Nenda!’ naye huenda, na mwingine, ‘Njoo!’ naye huja, na mtumwa wangu, ‘Fanya hili!’ naye hulifanya.” 9 Yesu aliposikia maneno hayo alishangazwa naye, akaugeukia umati uliokuwa ukimfuata na kusema: “Ninawaambia, hata katika Israeli sijaona imani kubwa kama hii.”+ 10 Na wale waliokuwa wametumwa waliporudi nyumbani, wakamkuta yule mtumwa amepona.+
11 Muda mfupi baadaye, Yesu akasafiri pamoja na wanafunzi wake na umati mkubwa kwenda jiji linaloitwa Naini. 12 Alipokaribia lango la jiji, tazama! kulikuwa na watu waliokuwa wamebeba maiti wakiipeleka nje, yule aliyekufa alikuwa mwana pekee,* na mama yake+ alikuwa mjane. Watu wengi kutoka jijini walikuwa pamoja na yule mwanamke. 13 Bwana alipomwona yule mjane akamsikitikia+ na kumwambia: “Acha kulia.”+ 14 Akakaribia na kuligusa jeneza,* nao wale waliolibeba wakasimama. Akasema: “Kijana, ninakuambia, inuka!”+ 15 Yule mfu akaketi akaanza kuongea, naye Yesu akamkabidhi kwa mama yake.+ 16 Basi wote wakaogopa, wakaanza kumtukuza Mungu wakisema: “Nabii mkuu ameinuliwa kati yetu,”+ na, “Mungu amewakumbuka watu wake.”+ 17 Habari hizo kumhusu Yesu zikaenea katika Yudea yote na maeneo jirani.
18 Basi wanafunzi wa Yohana wakamjulisha mambo hayo yote.+ 19 Ndipo Yohana akawaita wawili kati ya wanafunzi wake akawatuma kwa Bwana wamuulize: “Je, wewe ndiye Yule Anayekuja,+ au tumtarajie mwingine?” 20 Walipofika kwa Yesu wakamwambia: “Yohana Mbatizaji alitutuma kwako tukuulize: ‘Je, wewe ndiye Yule Anayekuja au tumtarajie mwingine?’” 21 Wakati huohuo, Yesu akawaponya watu wenye magonjwa,+ maradhi hatari, na wenye roho waovu, na pia akawapa vipofu wengi zawadi ya kuona. 22 Kisha akawajibu: “Nendeni mkamwambie Yohana mambo mliyoona na kusikia. Vipofu wanaona,+ viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakaswa, viziwi wanasikia,+ wafu wanafufuliwa, na maskini wanahubiriwa habari njema.+ 23 Mwenye furaha ni mtu ambaye hapati ndani yangu sababu ya kukwaza.”+
24 Wajumbe wa Yohana walipoondoka, Yesu akaanza kuuambia umati kumhusu Yohana: “Mlienda nyikani kuona nini? Tete likitikiswa na upepo?+ 25 Basi, mlienda kuona nini? Mtu aliyevaa mavazi laini?*+ Kwa maana wale wanaovaa mavazi maridadi na kuishi maisha ya anasa hukaa katika nyumba za kifalme. 26 Basi kwa kweli, mlienda kuona nini? Nabii? Ndiyo, ninawaambia, mtu aliye zaidi ya nabii.+ 27 Huyu ndiye ambaye imeandikwa hivi kumhusu, ‘Tazama! Ninamtuma mjumbe wangu mbele yako,* ili akutayarishie njia mbele yako.’+ 28 Ninawaambia, kati ya wale waliozaliwa na wanawake hakuna aliye mkuu kuliko Yohana, lakini mtu mdogo zaidi katika Ufalme wa Mungu, ni mkuu kuliko Yohana.”+ 29 (Watu wote na wakusanya kodi waliposikia jambo hilo, wakamtangaza Mungu kuwa mwadilifu, kwa sababu walikuwa wamebatizwa kwa ubatizo wa Yohana.+ 30 Lakini Mafarisayo na wale wenye ujuzi wa Sheria walilipuuza shauri la* Mungu,+ kwa sababu hawakuwa wamebatizwa na Yohana.)
31 “Basi, nitawalinganisha watu wa kizazi hiki na nani, wanafanana na nani?+ 32 Wao ni kama watoto walioketi sokoni ambao wanaambiana kwa sauti kubwa, wakisema: ‘Tuliwapigia filimbi, lakini hamkucheza dansi; tuliomboleza, lakini hamkulia.’ 33 Vivyo hivyo, Yohana Mbatizaji hakuja akila mkate wala kunywa divai,+ lakini mnasema: ‘Ana roho mwovu.’ 34 Mwana wa binadamu amekuja akila na kunywa, lakini mnasema: ‘Tazama! yeye ni mlafi na mwenye mazoea ya kunywa divai, rafiki ya wakusanya kodi na watenda dhambi!’+ 35 Hata hivyo, hekima huthibitishwa* kuwa yenye uadilifu kupitia watoto wake wote.”*+
36 Mmoja wa Mafarisayo alikuwa akimwomba Yesu ale pamoja naye. Basi akaenda katika nyumba ya Farisayo huyo na akaketi mezani. 37 Tazama! mwanamke aliyejulikana jijini kuwa mtenda dhambi akapata habari kwamba Yesu alikuwa akila* katika nyumba ya Farisayo, naye akaja na chupa ya alabasta yenye mafuta ya marashi.+ 38 Akaketi miguuni pa Yesu, akalia na kulowesha miguu yake kwa machozi na kuifuta kwa nywele za kichwa chake. Pia, akaibusu kwa wororo miguu ya Yesu na kuipaka mafuta ya marashi. 39 Alipoona hivyo, yule Farisayo aliyemwalika akajiambia: “Kama kweli mtu huyu angekuwa nabii, angejua ni nani na ni mwanamke wa aina gani anayemgusa, kwamba ni mtenda dhambi.”+ 40 Lakini Yesu akamwambia: “Simoni, ninataka kukuambia jambo.” Akasema: “Sema, mwalimu!”
41 “Mtu fulani aliwakopesha watu wawili pesa, mmoja alikuwa na deni la dinari* 500, na mwingine 50. 42 Waliposhindwa kumlipa, akawasamehe kwa hiari wote wawili. Kwa hiyo, ni nani kati yao atakayempenda zaidi?” 43 Simoni akajibu: “Nadhani ni yule aliyesamehewa zaidi.” Akamwambia: “Umejibu vizuri.” 44 Ndipo akamgeukia yule mwanamke na kumwambia Simoni: “Unamwona mwanamke huyu? Niliingia katika nyumba yako; hukunipa maji ya kuosha miguu yangu. Lakini mwanamke huyu aliiosha miguu yangu kwa machozi yake na kuifuta kwa nywele zake. 45 Wewe hukunibusu, lakini mwanamke huyu hajaacha kuibusu miguu yangu kwa wororo tangu nilipoingia. 46 Hukunipaka mafuta kichwani, lakini mwanamke huyu ameipaka miguu yangu mafuta yenye marashi. 47 Kwa hiyo, ninakuambia ingawa dhambi zake ni nyingi,* amesamehewa,+ kwa sababu amependa sana. Lakini anayesamehewa kidogo, hupenda kidogo.” 48 Ndipo akamwambia mwanamke huyo: “Umesamehewa dhambi zako.”+ 49 Wale walioketi mezani pamoja naye wakaanza kuulizana: “Mtu huyu ni nani ambaye hata anasamehe dhambi?”+ 50 Lakini akamwambia yule mwanamke: “Imani yako imekuokoa;+ nenda kwa amani.”
8 Muda mfupi baadaye Yesu akasafiri kutoka jiji mpaka jiji na kijiji mpaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu.+ Wale 12 walikuwa pamoja naye, 2 na pia wanawake fulani waliotolewa roho waovu na kuponywa magonjwa, yaani: Maria aitwaye Magdalene, ambaye alitolewa roho waovu saba; 3 Yoana+ mke wa Kuza, msimamizi wa nyumba ya Herode; Susana; na wanawake wengine wengi waliokuwa wakiwahudumia kwa mali zao.+
4 Umati mkubwa na pia watu waliokuja kutoka majiji mbalimbali walipokusanyika, Yesu akawaambia mfano huu:+ 5 “Mpandaji alienda kupanda mbegu. Alipokuwa akipanda, mbegu fulani zikaanguka kando ya barabara zikakanyagwa-kanyagwa, na ndege wa angani wakazila.+ 6 Nyingine zikaanguka kwenye mwamba, na baada ya kuchipuka, zikakauka kwa kukosa maji.+ 7 Nyingine zikaanguka kwenye miiba, nayo miiba ikakua pamoja nazo na kuzisonga.+ 8 Lakini nyingine zikaanguka kwenye udongo mzuri, zikachipuka na kuzaa matunda mara 100 zaidi.”+ Baada ya kusema hayo, akasema kwa sauti kubwa: “Yule aliye na masikio ya kusikiliza, na asikilize.”+
9 Lakini wanafunzi wake wakamuuliza maana ya mfano huo.+ 10 Akawaambia: “Ninyi mmepewa uwezo wa kuelewa siri takatifu za Ufalme wa Mungu, lakini ninazungumza na wale wengine kwa mifano,+ ili ingawa wanatazama, watazame lakini wasione, na ingawa wanasikia, wasielewe.+ 11 Basi mfano huo unamaanisha hivi: Mbegu ni neno la Mungu.+ 12 Mbegu zilizoanguka kando ya barabara ni wale ambao husikia, kisha Ibilisi huja na kuliondoa lile neno mioyoni mwao ili wasiamini na kuokolewa.+ 13 Mbegu zilizoanguka kwenye mwamba ni wale ambao wanapolisikia neno hulipokea kwa shangwe, lakini hawana mizizi. Wanaamini kwa muda, hata hivyo wanapojaribiwa wanaanguka.+ 14 Mbegu zilizoanguka kwenye miiba, ni wale ambao wamesikia, lakini wanakengeushwa na mahangaiko, utajiri,+ na raha za maisha.+ Wao husongwa kabisa na hawakomai.+ 15 Nazo mbegu zilizoanguka kwenye udongo mzuri, ni wale wenye moyo mzuri na mwema,+ ambao baada ya kulisikia neno hulihifadhi na kuzaa matunda kwa uvumilivu.+
16 “Hakuna mtu anayewasha taa na kuifunika kwa chombo au kuiweka chini ya kitanda, bali huiweka kwenye kinara cha taa, ili iwaangazie wale wanaoingia.+ 17 Kwa maana hakuna jambo lolote lililofichwa ambalo halitafunuliwa, wala jambo lolote lililofunikwa kwa uangalifu ambalo halitajulikana na kuwa wazi.+ 18 Kwa hiyo, kazieni uangalifu jinsi mnavyosikiliza, kwa maana yule aliye na kitu ataongezewa,+ lakini yule asiye na kitu, hata kile anachowazia kwamba anacho kitachukuliwa.”+
19 Sasa mama yake na ndugu zake+ wakaja, lakini hawakuweza kumfikia Yesu kwa sababu ya umati.+ 20 Basi akaambiwa: “Mama yako na ndugu zako wamesimama nje, wanataka kukuona.” 21 Akawajibu: “Mama yangu na ndugu zangu ni hawa wanaosikia neno la Mungu na kulitenda.”+
22 Siku moja, Yesu na wanafunzi wake walipanda mashua, naye akawaambia: “Tuvuke twende ng’ambo ya ziwa.” Basi wakaondoka.+ 23 Walipokuwa wakisafiri akalala usingizi. Dhoruba kali ya upepo ikatokea kwenye ziwa na mashua yao ikaanza kujaa maji ikakaribia kuzama.+ 24 Basi wakaenda kumwamsha na kusema: “Mwalimu, Mwalimu, tuko karibu kuangamia!” Ndipo akasimama, akaukemea upepo na mawimbi ya maji, nayo dhoruba ikatulia, kukawa shwari.+ 25 Kisha akawauliza: “Kwa nini hamna imani?” Lakini wakaogopa na kushangaa, wakaambiana: “Kwa kweli, mtu huyu ni nani? Kwa maana anaamuru upepo na maji, navyo vinamtii.”+
26 Wakafika pwani ya eneo la Wagerasene,+ lililo ng’ambo ya Galilaya. 27 Yesu alipotoka kwenye mashua akakutana na mwanamume fulani kutoka jijini aliyekuwa na roho mwovu. Hakuwa amevaa nguo kwa muda mrefu, na hakuwa akiishi katika nyumba bali aliishi makaburini.*+ 28 Alipomwona Yesu, akapaza kilio na kuanguka chini mbele yake, akasema kwa sauti kubwa: “Kwa nini unanisumbua, Yesu, Mwana wa Mungu Aliye Juu Zaidi? Ninakuomba, usinitese.”+ 29 (Kwa maana Yesu alikuwa akimwagiza huyo roho mwovu amtoke. Kwa sababu alikuwa amemshika mtu huyo mara nyingi,*+ naye alifungwa mara kwa mara kwa minyororo na pingu na kuwekwa chini ya ulinzi, lakini alivunja vifungo hivyo na yule roho mwovu akampeleka mahali pasipo na watu.) 30 Yesu akamuuliza: “Jina lako ni nani?” Akajibu: “Kikosi,” kwa sababu alikuwa ameingiwa na roho wengi waovu. 31 Nao wakaendelea kumsihi asiwaamuru waende katika shimo refu lisilo na mwisho.*+ 32 Sasa kulikuwa na kundi kubwa la nguruwe+ waliokuwa wakila mlimani, basi wakamsihi awaruhusu waingie ndani ya nguruwe hao, naye akawaruhusu.+ 33 Ndipo wale roho waovu wakamtoka mtu huyo na kuingia ndani ya wale nguruwe, kisha lile kundi likatimua mbio, likaruka poromoko,* likazama ndani ya ziwa na kufa maji. 34 Wachungaji walipoona kilichotokea, wakakimbia na kupeleka habari hizo jijini na mashambani.
35 Ndipo watu wakaenda kuona kilichotokea. Wakamjia Yesu na kumkuta yule mtu aliyetokwa na roho waovu ameketi miguuni pa Yesu, akiwa amevaa nguo na akiwa na akili timamu, nao wakaogopa. 36 Wale walioona jambo hilo wakawasimulia jinsi yule mtu aliyekuwa na roho waovu alivyoponywa. 37 Kisha watu wengi kutoka nchi ya Wagerasene wakamwomba Yesu aondoke, kwa sababu walikuwa wameogopa sana. Ndipo akapanda mashua ili aondoke. 38 Hata hivyo, yule mwanamume aliyetokwa na roho waovu akaendelea kumsihi aende pamoja naye, lakini Yesu hakumruhusu, akamwambia:+ 39 “Rudi nyumbani na uendelee kusimulia mambo ambayo Mungu amekutendea.” Basi akarudi, akitangaza katika jiji lote mambo ambayo Yesu alimtendea.
40 Yesu aliporudi, umati ukampokea kwa fadhili, kwa maana wote walikuwa wakimtarajia.+ 41 Lakini tazama! mwanamume anayeitwa Yairo akaja, alikuwa ofisa msimamizi wa sinagogi. Akajiangusha miguuni pa Yesu akaanza kumsihi aende nyumbani kwake,+ 42 kwa sababu binti yake wa pekee,* mwenye umri wa miaka 12 hivi, alikuwa karibu kufa.
Yesu alipokuwa akienda umati ukamsonga. 43 Kulikuwa na mwanamke aliyekuwa na mtiririko wa damu+ kwa miaka 12, na hakuwa amepata mtu wa kumponya.+ 44 Akaja kutoka nyuma na kugusa upindo wa vazi lake la nje,+ na mara moja akaacha kutokwa damu. 45 Ndipo Yesu akauliza: “Ni nani aliyenigusa?” Wote walipokuwa wakikana, Petro akasema: “Mwalimu, umati umekuzunguka na kukusonga.”+ 46 Lakini Yesu akasema: “Mtu fulani amenigusa, kwa maana ninajua nguvu+ zimenitoka.” 47 Yule mwanamke alipoona kwamba hakuepuka kutambuliwa, akaja akitetemeka na kuanguka chini mbele yake, akaeleza mbele ya watu wote sababu iliyomfanya amguse na jinsi alivyoponywa mara moja. 48 Lakini Yesu akamwambia: “Binti yangu, imani yako imekuponya. Nenda kwa amani.”+
49 Alipokuwa bado akizungumza, mwakilishi wa yule ofisa msimamizi wa sinagogi akaja na kusema: “Binti yako amekufa, usiendelee kumsumbua Mwalimu.”+ 50 Yesu aliposikia hilo akamwambia: “Usiogope, uwe tu na imani, naye ataokolewa.”+ 51 Alipofika kwenye nyumba hiyo, hakumruhusu yeyote aingie pamoja naye ila Petro, Yohana, Yakobo, na wazazi wa yule msichana. 52 Lakini watu wote walikuwa wakilia na kujipigapiga kwa huzuni kwa sababu ya yule msichana. Basi akawaambia: “Acheni kulia,+ kwa maana hajafa bali amelala usingizi.”+ 53 Ndipo wakaanza kumcheka kwa dharau, kwa sababu walijua amekufa. 54 Lakini akamshika mkono na kumwita: “Mtoto, inuka!”+ 55 Roho+ yake ikarudi* naye akasimama mara moja,+ kisha Yesu akaagiza apewe chakula. 56 Basi, wazazi wake wakafurahi sana, lakini Yesu akawaagiza wasimwambie mtu yeyote kilichotukia.+
9 Ndipo akawaita pamoja wale 12, akawapa nguvu na mamlaka ya kufukuza roho wote waovu+ na kuponya magonjwa.+ 2 Kisha akawatuma kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu na kuponya, 3 akawaambia: “Msibebe chochote kwa ajili ya safari, wala fimbo wala mfuko wa chakula wala mkate wala pesa;* wala msiwe na mavazi mawili.*+ 4 Lakini mtakapoingia katika nyumba yoyote, kaeni humo mpaka mtakapoondoka huko.+ 5 Popote ambapo watu hawatawakaribisha, mnapotoka katika jiji hilo kung’uteni mavumbi yaliyo kwenye miguu yenu ili uwe ushahidi dhidi yao.”+ 6 Kisha wakaenda katika eneo hilo kutoka kijiji mpaka kijiji, wakitangaza habari njema na kuponya wagonjwa kila mahali.+
7 Basi Herode* mtawala wa wilaya* aliposikia kuhusu mambo yaliyokuwa yakitukia, akashikwa na wasiwasi sana kwa sababu watu walikuwa wakisema Yohana alikuwa amefufuliwa kutoka kwa wafu,+ 8 lakini wengine walikuwa wakisema Eliya alikuwa ametokea, na wengine mmoja wa manabii wa kale alikuwa amefufuliwa.+ 9 Herode akasema: “Yohana nilimkata kichwa.+ Basi, ni nani huyu ninayesikia habari hizi kumhusu?” Kwa hiyo alitamani kumwona.+
10 Mitume waliporudi, wakamsimulia Yesu mambo yote waliyokuwa wamefanya.+ Ndipo akaondoka nao na kwenda faraghani katika jiji linaloitwa Bethsaida.+ 11 Lakini umati ulipojua, ukamfuata. Yesu akawapokea kwa fadhili na kuanza kuwaambia kuhusu Ufalme wa Mungu, naye akawaponya wale waliohitaji kuponywa.+ 12 Ilipokaribia jioni, wale 12 wakaja na kumwambia Yesu: “Uambie umati uondoke, waende vijijini na mashambani ili wakatafute chakula na mahali pa kulala, kwa sababu mahali hapa hapana watu.”+ 13 Lakini akawaambia: “Ninyi wapeni chakula.”+ Wakasema: “Tuna mikate mitano tu na samaki wawili, labda twende tukawanunulie watu hawa wote chakula.” 14 Kwa kweli, kulikuwa na karibu wanaume 5,000. Lakini akawaambia wanafunzi wake: “Waambieni waketi katika vikundi vya watu hamsini hamsini.” 15 Wakafanya hivyo, na kila mtu akaketi. 16 Akachukua ile mikate mitano na wale samaki wawili, akatazama mbinguni na kuvibariki. Kisha akavimega, akaanza kuwapa wanafunzi ili wawape watu. 17 Basi wote wakala wakashiba, nao wakakusanya chakula kilichobaki na kujaza vikapu 12.+
18 Baadaye, alipokuwa akisali akiwa peke yake, wanafunzi wakaja, naye akawauliza: “Umati unasema mimi ni nani?”+ 19 Wakamjibu: “Yohana Mbatizaji, lakini wengine wanasema Eliya, na bado wengine husema mmoja wa manabii wa kale amefufuliwa.”+ 20 Ndipo akawauliza: “Hata hivyo, ninyi mnasema mimi ni nani?” Petro akajibu: “Kristo wa Mungu.”+ 21 Ndipo akawaagiza kwa uthabiti wasimwambie mtu yeyote jambo hilo,+ 22 lakini akasema: “Lazima Mwana wa binadamu apatwe na mateso mengi, akataliwe na wazee, wakuu wa makuhani, na waandishi, kisha atauawa,+ na siku ya tatu atafufuliwa.”+
23 Ndipo akawaambia wote: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe,+ aubebe mti* wake wa mateso siku baada ya siku na aendelee kunifuata.+ 24 Kwa maana yeyote anayetaka kuuokoa uhai wake* ataupoteza, lakini yeyote anayeupoteza uhai wake* kwa ajili yangu ndiye atakayeuokoa.+ 25 Kwa kweli, mtu atapata faida gani akiupata ulimwengu wote lakini apoteze uhai wake au apate hasara?+ 26 Kwa maana yeyote atakayenionea aibu mimi na maneno yangu, Mwana wa binadamu atamwonea aibu mtu huyo, atakapokuja katika utukufu wake, na wa Baba, na wa malaika watakatifu.+ 27 Lakini kwa kweli ninawaambia, kuna baadhi ya wale waliosimama hapa ambao hawataonja kifo kamwe kabla ya kuuona Ufalme wa Mungu.”+
28 Kwa hakika, karibu siku nane baada ya Yesu kusema maneno hayo, alienda mlimani na Petro, Yohana, na Yakobo ili kusali.+ 29 Alipokuwa akisali uso wake ukabadilika, mavazi yake yakawa meupe na kuanza kumetameta. 30 Na tazama! wanaume wawili walikuwa wakizungumza naye; walikuwa Musa na Eliya. 31 Walitokea wakiwa na utukufu na wakaanza kuongea kuhusu kuondoka kwake, ambako kungetimizwa huko Yerusalemu.+ 32 Petro na wenzake walikuwa wamelemewa na usingizi, lakini walipoamka kabisa waliuona utukufu wa Yesu+ na wanaume wawili waliokuwa wamesimama pamoja naye. 33 Wale wanaume wawili walipokuwa wakiondoka, Petro akamwambia Yesu: “Mwalimu, ni vizuri sisi tuwe hapa. Basi, tutasimamisha mahema matatu, moja lako, moja la Musa, na moja la Eliya.” Hakujua alichokuwa akisema. 34 Lakini alipokuwa akisema mambo haya, wingu likatokea na kuanza kuwafunika. Walipokuwa wakifunikwa na wingu, wakaogopa. 35 Kisha sauti+ ikasikika katika lile wingu ikisema: “Huyu ni Mwanangu aliyechaguliwa.+ Msikilizeni.”+ 36 Walipokuwa wakisikia ile sauti, wakamwona Yesu akiwa peke yake. Lakini wakakaa kimya na katika siku hizo hawakumwambia mtu yeyote lolote kati ya mambo waliyoona.+
37 Siku iliyofuata, waliposhuka kutoka mlimani, Yesu alikutana na umati mkubwa.+ 38 Na tazama! mtu fulani katika umati akasema kwa sauti kubwa: “Mwalimu, ninakuomba umwangalie mwanangu, kwa sababu yeye ni mwanangu wa pekee.+ 39 Tazama! roho mwovu humshika, naye hupiga kelele ghafla, na humfanya agaegae na kutokwa na povu mdomoni, naye hamtoki upesi mpaka anapomjeruhi. 40 Niliwaomba wanafunzi wako wamfukuze, lakini wakashindwa.” 41 Yesu akajibu: “Enyi kizazi kisicho na imani na kilichopotoka,+ nitaendelea kuwa pamoja nanyi na kuwavumilia mpaka lini? Mlete mwanao hapa.”+ 42 Lakini alipokuwa akikaribia, yule roho mwovu akamwangusha na kumfanya agaegae sana. Hata hivyo, Yesu akamkemea yule roho mwovu na kumponya mvulana huyo, kisha akamkabidhi kwa baba yake. 43 Wote wakashangazwa na ukuu wa nguvu za Mungu.
Walipokuwa bado wanashangaa kuhusu mambo yote aliyokuwa akifanya, akawaambia wanafunzi wake: 44 “Sikilizeni kwa makini na mkumbuke maneno haya, kwa maana Mwana wa binadamu atasalitiwa mikononi mwa watu.”+ 45 Lakini hawakuelewa maneno hayo. Kwa kweli, yalifichwa ili wasiyafahamu, nao waliogopa kumuuliza kuhusu maneno hayo.
46 Kisha wanafunzi wakaanza kubishana kuhusu aliyekuwa mkuu zaidi kati yao.+ 47 Yesu, akijua mawazo ya mioyo yao, akachukua mtoto na kumsimamisha kando yake, 48 akawaambia: “Yeyote anayempokea mtoto huyu kwa msingi wa jina langu ananipokea mimi pia, na yeyote anayenipokea, anampokea pia Yule aliyenituma.+ Kwa maana anayejiendesha kama mdogo zaidi kati yenu nyote ndiye mkuu.”+
49 Yohana akasema: “Mwalimu, tulimwona mtu fulani akifukuza roho waovu kwa kutumia jina lako, tukajaribu kumzuia, kwa sababu hafuatani nasi.”+ 50 Lakini Yesu akamwambia: “Msijaribu kumzuia, kwa maana yeyote asiyewapinga yuko upande wenu.”
51 Wakati ulipokuwa ukikaribia* wa Yesu kwenda mbinguni,+ akaazimia kwenda Yerusalemu. 52 Basi akawatuma wajumbe wamtangulie. Wakaenda katika kijiji kimoja cha Wasamaria, ili wafanye matayarisho kwa ajili yake. 53 Lakini hawakumpokea,+ kwa sababu alikuwa ameazimia* kwenda Yerusalemu. 54 Wanafunzi Yakobo na Yohana+ walipoona hilo wakauliza: “Bwana unataka tuagize moto utoke mbinguni uwaangamize?”+ 55 Lakini Yesu akageuka akawakemea. 56 Basi wakaenda kwenye kijiji kingine.
57 Wakiwa njiani, mtu fulani akamwambia Yesu: “Nitakufuata popote utakapoenda.” 58 Lakini Yesu akamwambia: “Mbweha wana mapango na ndege wa angani wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali pa kulaza kichwa chake.”+ 59 Kisha akamwambia mtu mwingine: “Njoo, uwe mfuasi wangu.” Mtu huyo akasema: “Bwana, niruhusu kwanza niende nikamzike baba yangu.”+ 60 Yesu akamwambia: “Waache wafu+ wawazike wafu wao, lakini wewe nenda ukatangaze Ufalme wa Mungu kila mahali.”+ 61 Mtu mwingine akamwambia: “Bwana nitakufuata, lakini niruhusu kwanza nikawaage watu wa nyumbani kwangu.” 62 Yesu akamwambia: “Yeyote anayeshika jembe la ng’ombe na kutazama vitu vilivyo nyuma+ hastahili Ufalme wa Mungu.”+
10 Baada ya mambo hayo Bwana akachagua wengine 70, akawatuma wawili wawili+ wamtangulie katika kila jiji na kila mahali ambako yeye mwenyewe angeenda. 2 Kisha akawaambia: “Ndiyo, mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.+ 3 Nendeni! Tazama! Ninawatuma kama wanakondoo katikati ya mbwamwitu.+ 4 Msibebe mkoba wa pesa wala mfuko wa chakula wala viatu,+ na msimsalimu* mtu yeyote njiani. 5 Mkiingia katika nyumba yoyote, kwanza semeni: ‘Nyumba hii na iwe na amani.’+ 6 Na kama humo kuna rafiki wa amani, amani yenu itakaa naye. Lakini ikiwa hakuna, itawarudia. 7 Basi kaeni katika nyumba hiyo,+ na mle na kunywa watakachowaandalia,+ kwa maana mfanyakazi anastahili mshahara wake.+ Msihame kutoka nyumba mpaka nyumba.
8 “Pia, mkiingia katika jiji nanyi mkaribishwe, kuleni watakachowapa, 9 na mponye wagonjwa walio huko na kuwaambia: ‘Ufalme wa Mungu umekuja karibu nanyi.’+ 10 Lakini mkiingia katika jiji nao wasiwakaribishe, nendeni kwenye barabara zake kuu na kusema: 11 ‘Hata mavumbi ya jiji lenu yaliyo kwenye miguu yetu tunayafuta dhidi yenu.+ Hata hivyo jueni kwamba Ufalme wa Mungu umekaribia.’ 12 Ninawaambia kwamba katika siku hiyo, itakuwa afadhali zaidi kwa Sodoma kuliko kwa jiji hilo.+
13 “Ole wako, Korazini! Ole wako, Bethsaida! kwa sababu kama matendo yenye nguvu yaliyofanywa kwenu yangefanywa huko Tiro na Sidoni, wangekuwa wametubu zamani, wakiwa wamevaa nguo za magunia na kuketi kwenye majivu.+ 14 Kwa hiyo, wakati wa hukumu itakuwa afadhali zaidi kwa Tiro na Sidoni kuliko kwenu. 15 Nawe Kapernaumu, je, utainuliwa mpaka mbinguni? Utashuka mpaka Kaburini!*
16 “Yeyote anayewasikiliza ninyi ananisikiliza mimi pia.+ Na yeyote anayewapuuza ninyi ananipuuza mimi pia. Isitoshe, yeyote anayenipuuza mimi anampuuza pia Yule aliyenituma.”+
17 Ndipo wale 70 wakarudi wakiwa na shangwe, wakisema: “Bwana, hata tunawatiisha roho waovu kwa kutumia jina lako.”+ 18 Ndipo akawaambia: “Ninamwona Shetani akiwa tayari ameanguka+ kutoka mbinguni kama radi. 19 Tazama! Nimewapa mamlaka ya kukanyaga nyoka na nge, na juu ya nguvu zote za adui,+ na hakuna kitu chochote kitakachowadhuru. 20 Hata hivyo, msishangilie kwa sababu mnawatiisha roho waovu, bali shangilieni kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.”+ 21 Saa ileile akawa na shangwe kubwa kupitia roho takatifu na kusema: “Ninakusifu hadharani, Baba, Bwana wa mbingu na dunia, kwa sababu umewaficha kwa uangalifu mambo haya wenye hekima na wenye akili+ nawe umeyafunua kwa watoto wadogo. Ndiyo, Ee Baba, kwa sababu umekubali iwe hivyo.+ 22 Baba yangu amenikabidhi vitu vyote, na hakuna mtu anayemjua Mwana isipokuwa Baba, wala hakuna anayemjua Baba isipokuwa Mwana,+ na yeyote ambaye Mwana anapenda kumfunulia.”+
23 Ndipo akawageukia wanafunzi wake faraghani na kuwaambia: “Yenye furaha ni macho yanayoona mambo mnayoona.+ 24 Kwa maana ninawaambia, manabii na wafalme wengi walitamani kuona mambo mnayoona lakini hawakuyaona,+ na kusikia mambo mnayosikia lakini hawakuyasikia.”
25 Tazama! mtu fulani mwenye ujuzi wa Sheria akasimama ili amjaribu, akamuuliza: “Mwalimu, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?”+ 26 Yesu akamuuliza: “Ni mambo gani yameandikwa katika Sheria? Wewe unasomaje?” 27 Akajibu: “‘Lazima umpende Yehova* Mungu wako kwa moyo wako wote kwa nafsi* yako yote kwa nguvu zako zote na kwa akili yako yote’+ na ‘umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.’”+ 28 Akamwambia: “Umejibu vizuri; endelea kufanya hivyo nawe utapata uzima.”+
29 Lakini, akitaka kujionyesha kuwa mwadilifu,+ mtu huyo akamuuliza Yesu: “Kwa kweli jirani yangu ni nani?” 30 Yesu akamjibu: “Mtu fulani alikuwa akishuka kutoka Yerusalemu kwenda Yeriko akavamiwa na wezi, wakamvua nguo, wakampiga, kisha wakamwacha akiwa karibu kufa. 31 Ikatukia kwamba kuhani fulani alikuwa akishuka katika barabara hiyo, lakini alipomwona yule mtu akapita upande mwingine wa barabara. 32 Vivyo hivyo, Mlawi alipofika mahali hapo na kumwona, akapita upande mwingine wa barabara. 33 Lakini Msamaria+ fulani aliyekuwa akisafiri kwenye barabara hiyo alipomwona, akamsikitikia. 34 Basi akamkaribia akayamwagia majeraha yake mafuta na divai, kisha akayafunga. Akampandisha kwenye punda wake akampeleka kwenye nyumba ya wageni na kumtunza. 35 Siku iliyofuata akamlipa msimamizi wa nyumba hiyo dinari* mbili, akamwambia: ‘Mtunze, nami nitakulipa gharama zozote za ziada nitakaporudi.’ 36 Kati ya watu hao watatu, unafikiri ni nani aliyekuwa jirani+ ya mtu aliyevamiwa na wezi?” 37 Akajibu: “Ni yule aliyemtendea kwa rehema.”+ Ndipo Yesu akamwambia: “Nenda ukafanye vivyo hivyo.”+
38 Walipoendelea na safari, wakaingia katika kijiji fulani. Mwanamke aliyeitwa Martha+ akamkaribisha Yesu nyumbani kwake. 39 Martha alikuwa na dada aliyeitwa Maria, ambaye aliketi miguuni pa Bwana akisikiliza alichokuwa akisema.* 40 Lakini Martha alikengeushwa na kazi nyingi. Basi, akaja na kusema: “Bwana, hujali kwamba dada yangu ameniacha nishughulike peke yangu? Mwambie aje anisaidie.” 41 Bwana akamjibu: “Martha, Martha, unasumbuka na kuhangaikia mambo mengi. 42 Ni vitu vichache tu vinavyohitajiwa au kimoja tu. Maria alichagua fungu zuri,*+ nalo halitaondolewa kwake.”
11 Sasa alikuwa mahali fulani akisali, alipomaliza, mmoja wa wanafunzi wake akamwambia: “Bwana, tufundishe jinsi ya kusali, kama vile Yohana alivyowafundisha wanafunzi wake.”
2 Basi akawaambia: “Mnaposali, semeni, ‘Baba, jina lako na litakaswe.*+ Ufalme wako na uje.+ 3 Kila siku utupatie mkate wetu kulingana na mahitaji yetu.+ 4 Na utusamehe dhambi zetu,+ kwa maana sisi pia humsamehe kila mtu aliye na deni letu;+ na usituingize katika majaribu.’”+
5 Kisha akawaambia: “Ikiwa mmoja wenu ana rafiki, naye aende kwake katikati ya usiku na kumwambia, ‘Rafiki, nikopeshe mikate mitatu, 6 kwa sababu rafiki yangu amekuja kwangu kutoka safarini nami sina kitu cha kumpa.’ 7 Lakini yule aliye ndani amjibu: ‘Acha kunisumbua. Tayari mlango umefungwa, nami na watoto wangu tumelala. Siwezi kuamka nikupe chochote.’ 8 Ninawaambia ingawa hataamka na kumpa chochote kwa sababu yeye ni rafiki yake, kwa hakika ataamka na kumpa kwa sababu anaendelea+ kumwomba. 9 Basi ninawaambia, endeleeni kuomba,+ nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa.+ 10 Kwa maana kila mtu anayeomba hupokea,+ na kila mtu anayetafuta hupata, na kila mtu anayepiga hodi atafunguliwa. 11 Kwa kweli, ni baba gani kati yenu ambaye mwana wake akiomba samaki, atampa nyoka?+ 12 Au pia akiomba yai, atampa nge? 13 Kwa hiyo, ingawa ninyi ni waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi nzuri, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!”+
14 Baadaye alimfukuza roho mwovu aliye bubu.+ Roho huyo mwovu alipotoka, yule bubu akazungumza. Nao umati ukashangaa.+ 15 Lakini baadhi yao wakasema: “Anawafukuza roho waovu kwa nguvu za Beelzebuli,* mtawala wa roho waovu.”+ 16 Na wengine, ili kumjaribu, wakamwomba afanye ishara+ kutoka mbinguni. 17 Akijua mawazo yao,+ akawaambia: “Kila ufalme uliogawanyika dhidi yake wenyewe utaangamia, na nyumba iliyogawanyika dhidi yake yenyewe itaanguka. 18 Vivyo hivyo, ikiwa Shetani amegawanyika dhidi yake mwenyewe, ufalme wake utawezaje kusimama? Kwa maana mnasema ninafukuza roho waovu kupitia Beelzebuli. 19 Ikiwa ninawafukuza roho waovu kupitia Beelzebuli, wana wenu wanawafukuza kupitia nani? Hiyo ndiyo sababu watakuwa waamuzi wenu. 20 Lakini ikiwa ninawafukuza roho waovu kupitia kidole cha Mungu,+ kwa kweli Ufalme wa Mungu umewafikia ninyi ghafla.+ 21 Mtu mwenye nguvu aliye na silaha, anapolinda jumba lake, mali yake huwa salama. 22 Lakini mtu mwingine mwenye nguvu zaidi yake anapomshambulia na kumshinda, humnyang’anya silaha zake zote alizotegemea, naye hugawa vitu alivyompora. 23 Yeyote asiye upande wangu ananipinga, na yeyote asiyekusanya pamoja nami anatawanya.+
24 “Roho mwovu anapomtoka mtu, yeye hupitia maeneo yasiyo na maji akitafuta mahali pa kupumzika, lakini anapokosa yeye husema, ‘Nitarudi kwenye nyumba yangu niliyoihama.’+ 25 Anapofika hukuta nyumba ikiwa imefagiwa ikawa safi na kupambwa. 26 Kisha huenda na kuwaleta roho wengine saba walio waovu kuliko yeye, na baada ya kuingia ndani, wao hukaa humo. Basi hali ya mwisho ya mtu huyo huwa mbaya zaidi kuliko ya kwanza.”
27 Alipokuwa akisema mambo hayo mwanamke fulani katika umati akasema kwa sauti kubwa: “Lenye furaha ni tumbo lililokubeba wewe na matiti uliyonyonya!”+ 28 Lakini Yesu akasema: “Hapana, badala yake, wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!”+
29 Umati ulipozidi kuongezeka, akaanza kusema: “Kizazi hiki ni kiovu; kinatafuta ishara, lakini hakitapewa ishara yoyote isipokuwa ishara ya Yona.+ 30 Kwa maana kama vile Yona+ alivyokuwa ishara kwa Waninawi, ndivyo Mwana wa binadamu atakavyokuwa kwa kizazi hiki. 31 Malkia wa kusini+ atasimamishwa katika hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki naye atakihukumu kwa sababu alikuja kutoka miisho ya dunia ili asikie hekima ya Sulemani. Lakini tazama! hapa pana mtu mkuu kuliko Sulemani.+ 32 Watu wa Ninawi watasimama katika hukumu pamoja na kizazi hiki nao watakihukumu, kwa sababu walitubu Yona alipowahubiria.+ Lakini tazama! hapa pana mtu mkuu kuliko Yona. 33 Hakuna mtu anayewasha taa na kuificha au kuiweka chini ya kikapu,* bali huiweka kwenye kinara cha taa,+ ili iwaangazie wale wanaoingia. 34 Taa ya mwili ni jicho lako. Ikiwa jicho lako linakazia jambo hususa,* mwili wako wote utakuwa mwangavu;* lakini ikiwa lina wivu,* mwili wako utakuwa na giza.+ 35 Basi, uwe mwangalifu ili nuru iliyo ndani yako isiwe ni giza. 36 Kwa hiyo, ikiwa mwili wako wote ni mwangavu bila giza lolote, utakuwa mwangavu kama taa inapokuangazia kwa mwanga wake.”
37 Baada ya kusema hayo, Farisayo mmoja alimwomba ale pamoja naye. Basi Yesu akaingia na kuketi mezani. 38 Hata hivyo, Farisayo huyo akashangaa kuona kwamba Yesu hakunawa* kabla ya kula.+ 39 Lakini Bwana akamwambia: “Ninyi Mafarisayo, husafisha upande wa nje wa kikombe na sahani, lakini ndani yenu mmejaa pupa na uovu.+ 40 Enyi wapumbavu! Yule aliyetengeneza nje ndiye aliyetengeneza ndani pia, sivyo? 41 Lakini toeni vitu vilivyo ndani viwe zawadi za rehema,* na tazama! mtakuwa safi katika mambo mengine yote. 42 Lakini ole wenu Mafarisayo, kwa sababu mnatoa sehemu ya kumi ya mnanaa na mchicha na kila aina ya mboga,+ lakini mnapuuza haki na kumpenda Mungu! Mlipaswa kufanya mambo hayo, bila kupuuza yale mengine.+ 43 Ole wenu Mafarisayo, kwa sababu mnapenda viti vya mbele* katika masinagogi na kusalimiwa sokoni!+ 44 Ole wenu, kwa sababu ninyi ni kama makaburi* yasiyoonekana,*+ ambayo watu hutembea juu yake bila kujua!”
45 Mtu fulani mwenye ujuzi wa Sheria akamwambia: “Mwalimu, unaposema mambo hayo, unatutukana sisi pia.” 46 Ndipo akasema: “Ole wenu pia ninyi mlio na ujuzi wa Sheria, kwa sababu mnawatwika watu mizigo mizito, lakini ninyi wenyewe hamwigusi hata kwa kidole kimoja!+
47 “Ole wenu, kwa sababu mnajenga makaburi* ya manabii ambao mababu zenu waliwaua!+ 48 Hakika ninyi ni mashahidi wa matendo ya mababu zenu nanyi mnakubaliana nao, kwa sababu waliwaua manabii+ nanyi mnajenga makaburi yao. 49 Kwa sababu hiyo hekima ya Mungu ilisema: ‘Nitawatuma manabii na mitume kwao, lakini watawaua na kuwatesa baadhi yao, 50 ili damu ya manabii wote iliyomwagwa tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu idaiwe kutoka kwa kizazi hiki,+ 51 kuanzia damu ya Abeli+ mpaka damu ya Zekaria, aliyeuawa kati ya madhabahu na ile nyumba.’*+ Ndiyo, ninawaambia, kizazi hiki kitadaiwa* damu hiyo.
52 “Ole wenu ninyi wenye ujuzi wa Sheria, kwa sababu mliuondoa ufunguo wa ujuzi. Ninyi hamkuingia, na mnawazuia wale wanaoingia!”+
53 Basi alipotoka hapo, waandishi na Mafarisayo wakaanza kumsonga sana na kumuuliza maswali mengi, 54 wakimtega ili wamnase kwa maneno yake.+
12 Wakati huo, maelfu ya watu walikusanyika hata wakawa wanakanyagana, Yesu akaanza kuzungumza kwanza na wanafunzi wake: “Jihadharini na chachu ya Mafarisayo, ambayo ni unafiki.+ 2 Lakini hakuna jambo lolote lililofunikwa kwa uangalifu ambalo halitafunuliwa, na hakuna siri yoyote ambayo haitafichuliwa.+ 3 Kwa hiyo, mambo mnayosema gizani yatasikiwa nuruni, na mambo mnayonong’ona katika vyumba vya faragha yatahubiriwa juu ya paa za nyumba. 4 Isitoshe, ninawaambia ninyi, rafiki zangu,+ msiwaogope wale wanaoua mwili na baada ya hilo hawawezi kufanya jambo lolote zaidi.+ 5 Lakini nitawaonyesha yule mnayepaswa kumwogopa: Mwogopeni yule ambaye baada ya kuua ana mamlaka ya kutupa ndani ya Gehena.*+ Ndiyo, ninawaambia, mwogopeni Huyo.+ 6 Shore watano huuzwa kwa sarafu mbili za thamani ndogo,* sivyo? Na bado Mungu hamsahau* hata mmoja.+ 7 Lakini hata nywele zote za vichwa vyenu zimehesabiwa.+ Msiogope; ninyi ni wenye thamani kuliko shore wengi.+
8 “Ninawaambia, kila mtu anayenikiri mbele ya watu,+ Mwana wa binadamu pia atamkiri mbele ya malaika wa Mungu.+ 9 Lakini yeyote anayenikana mbele ya watu atakanwa mbele ya malaika wa Mungu.+ 10 Na kila mtu anayesema neno baya kumhusu Mwana wa binadamu atasamehewa, lakini yeyote anayeikufuru roho takatifu hatasamehewa.+ 11 Mtakapopelekwa mbele ya makusanyiko ya watu wote,* maofisa wa serikali, na mamlaka, msihangaike kuhusu jinsi mtakavyojitetea au jambo mtakalosema,+ 12 kwa maana saa hiyohiyo roho takatifu itawafundisha mambo mnayopaswa kusema.”+
13 Kisha mtu fulani katika umati akamwambia: “Mwalimu, mwambie ndugu yangu tugawane urithi.” 14 Akamwambia: “Ni nani aliyeniweka niwe mwamuzi au mpatanishi kati yenu wawili?” 15 Ndipo akawaambia: “Endeleeni kufungua macho yenu na mjilinde na kila aina ya pupa,*+ kwa sababu hata mtu anapokuwa na vitu vingi, uhai wake hautokani na vitu alivyo navyo.”+ 16 Ndipo akawaambia mfano huu: “Shamba la tajiri fulani lilizaa vizuri. 17 Basi akaanza kuwaza moyoni, ‘Nitafanya nini kwa sababu sina mahali pa kuhifadhi mazao yangu?’ 18 Kisha akasema, ‘Nitafanya hivi:+ Nitabomoa maghala yangu na kujenga makubwa zaidi, kisha nitahifadhi humo nafaka yangu na vitu vyangu vyote, 19 kisha nitajiambia:* “Una* vitu vingi vizuri ulivyokusanya kwa miaka mingi; starehe, ule, unywe, na ujifurahishe.”’ 20 Lakini Mungu akamwambia, ‘Wewe mpumbavu, usiku huu wanautaka uhai wako.* Basi, vitu ulivyohifadhi vitakuwa vya nani?’+ 21 Hivyo ndivyo huwa kwa mtu anayejiwekea hazina lakini si tajiri kwa Mungu.”+
22 Kisha akawaambia wanafunzi wake: “Ndiyo sababu ninawaambia, acheni kuhangaikia uhai wenu* kuhusu kile mtakachokula au miili yenu kuhusu kile mtakachovaa.+ 23 Kwa maana uhai una* thamani kuliko chakula na mwili kuliko mavazi. 24 Waangalieni kunguru: Hawapandi mbegu wala hawavuni; hawana bohari wala ghala; lakini Mungu huwalisha.+ Je, ninyi si wenye thamani kuliko ndege?+ 25 Ni nani kati yenu ambaye kwa kuhangaika anaweza kurefusha uhai wake kwa mkono* mmoja? 26 Basi, kama hamwezi kufanya jambo dogo kama hilo, kwa nini mhangaikie yale mambo mengine?+ 27 Angalieni jinsi mayungiyungi* yanavyokua: Hayafanyi kazi wala hayasokoti; lakini ninawaambia hata Sulemani katika utukufu wake wote hakupambwa kama maua hayo.+ 28 Basi, ikiwa Mungu huivika hivyo mimea ya shambani, ambayo ipo leo na kesho hutupwa ndani ya jiko, je, hatawavika vizuri zaidi ninyi wenye imani ndogo? 29 Basi acheni kutafuta kile mtakachokula au mtakachokunywa, na acheni kuhangaika kwa wasiwasi;+ 30 kwa maana mataifa yanatafuta vitu hivi vyote kwa bidii, lakini Baba yenu anajua mnahitaji vitu hivi.+ 31 Badala yake, endeleeni kuutafuta Ufalme wake, nanyi mtaongezewa vitu hivyo.+
32 “Msiogope, ninyi kundi dogo,+ kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa Ufalme.+ 33 Uzeni mali zenu na kutoa zawadi za rehema.*+ Tengenezeni mikoba ya pesa isiyochakaa, hazina isiyopungua huko mbinguni,+ ambako mwizi hawezi kufika wala nondo* hali. 34 Kwa maana mahali ilipo hazina yenu, ndipo mioyo yenu itakapokuwa.
35 “Vaeni mavazi, muwe tayari*+ na mwashe taa zenu,+ 36 nanyi muwe kama watu wanaomsubiri bwana wao arudi+ kutoka kwenye karamu ya ndoa,+ ili atakapokuja na kupiga hodi wamfungulie mara moja. 37 Wenye furaha ni watumwa ambao bwana wao akija atawakuta wakikesha! Kwa kweli ninawaambia, atavaa vazi la mhudumu* na kuwaambia waketi mezani naye atakuja na kuwahudumia. 38 Akija katika kesha la pili,* au hata kesha la tatu,* na kuwakuta wakiwa tayari, watakuwa wenye furaha! 39 Lakini jueni jambo hili, ikiwa mwenye nyumba angejua saa ambayo mwizi angekuja, hangeruhusu nyumba yake ivunjwe.+ 40 Ninyi pia, endeleeni kuwa tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja saa msiyotazamia.”+
41 Ndipo Petro akamuuliza: “Bwana, unatuambia sisi tu mfano huo au watu wote pia?” 42 Bwana akasema: “Kwa kweli ni nani msimamizi* mwaminifu, mwenye busara,* ambaye bwana wake atamweka asimamie watumishi* wake na kuendelea kuwapa kipimo chao cha chakula kwa wakati unaofaa?+ 43 Mwenye furaha ni mtumwa huyo, ikiwa bwana wake atakapokuja atamkuta akifanya hivyo! 44 Kwa kweli ninawaambia, atamweka rasmi asimamie mali zake zote. 45 Lakini ikiwa mtumwa huyo atasema moyoni mwake, ‘Bwana wangu anakawia kuja,’ naye aanze kuwapiga watumishi wa kiume na wa kike na kula na kunywa na kulewa,+ 46 bwana wa mtumwa huyo atakuja siku asiyomtazamia na katika saa asiyoijua, naye atamwadhibu kwa ukali na kumweka pamoja na wasio waaminifu. 47 Mtumwa huyo aliyeelewa mapenzi ya bwana wake lakini hakujitayarisha wala kufanya alichoambiwa* atapigwa sana.+ 48 Lakini yule ambaye hakuelewa na hivyo akafanya mambo yanayostahili adhabu atapigwa kidogo. Kwa kweli, kila mtu ambaye alipewa mengi atadaiwa mengi, na yule aliyewekwa kusimamia mengi, atadaiwa mengi kuliko ilivyo kawaida.+
49 “Nilikuja kuwasha moto duniani, na kama tayari umewaka, ninahitaji nini kingine? 50 Kwa kweli, kuna ubatizo ninaopaswa kubatizwa, na ninataabika sana mpaka umalizike!+ 51 Je, mnafikiri nilikuja kuleta amani duniani? Hapana, si amani bali mgawanyiko.+ 52 Kuanzia sasa kutakuwa na watu watano katika nyumba moja waliogawanyika, watatu dhidi ya wawili na wawili dhidi ya watatu. 53 Watagawanyika, baba dhidi ya mwana, mwana dhidi ya baba, mama dhidi ya binti, binti dhidi ya mama, mama mkwe dhidi ya binti mkwe, na binti mkwe dhidi ya mama mkwe.”+
54 Kisha akauambia umati: “Mnapoona wingu likitokea magharibi, mara moja mnasema, ‘Kutakuwa na dhoruba,’ na inakuwa hivyo. 55 Nanyi mnapoona upepo wa kusini ukivuma, ninyi husema, ‘Kutakuwa na joto sana,’ na inakuwa hivyo. 56 Wanafiki, mnajua jinsi ya kuchunguza dunia na anga, lakini kwa nini hamjui jinsi ya kuchunguza kinachotendeka wakati huu?+ 57 Kwa nini hamtambui pia mambo yaliyo ya uadilifu? 58 Kwa mfano, unapoenda kwa mtawala pamoja na mtu anayekushtaki, anza kusuluhisha mambo pamoja naye mkiwa njiani, ili asikupeleke mbele ya hakimu, naye hakimu akukabidhi kwa ofisa wa mahakama, naye ofisa wa mahakama akutupe gerezani.+ 59 Ninakuambia, hakika hutatoka humo mpaka utakapolipa sarafu* yako ndogo ya mwisho.”
13 Wakati huo, watu fulani waliokuwa hapo walimwambia Yesu kuhusu Wagalilaya ambao Pilato alikuwa amechanganya damu yao na dhabihu zao. 2 Akawaambia: “Je, mnafikiri Wagalilaya hao walikuwa watenda dhambi wabaya zaidi kuliko Wagalilaya wengine wote kwa sababu walipatwa na mambo hayo? 3 Hapana. Ninawaambia msipotubu, nyote mtaangamizwa vivyo hivyo.+ 4 Au wale 18 walioangukiwa na mnara huko Siloamu wakafa, je, mnafikiri walikuwa na hatia kuliko watu wengine wote wanaoishi Yerusalemu? 5 Hapana, ninawaambia; msipotubu, ninyi pia mtaangamizwa kama wao.”
6 Kisha akawaambia mfano huu: “Mtu fulani alikuwa na mtini uliopandwa katika shamba lake la mizabibu, akaenda kutafuta matunda kwenye mti huo lakini hakupata.+ 7 Ndipo akamwambia mtunza-mizabibu, ‘Kwa miaka mitatu nimekuwa nikija kutafuta matunda kwenye mtini huu, lakini sijayapata. Ukate! Kwa nini uendelee kuharibu ardhi?’ 8 Akamjibu, ‘Bwana, uache kwa mwaka mwingine mmoja niupalilie na kuutia mbolea. 9 Ukizaa matunda wakati ujao, vema; la sivyo, utaukata.’”+
10 Sasa Yesu alikuwa akifundisha katika sinagogi siku ya Sabato. 11 Na tazama! hapo palikuwa na mwanamke aliyekuwa na roho ya udhaifu* kwa miaka 18, mwili wake ulikuwa umepindika na hangeweza kusimama wima. 12 Yesu alipomwona, akamwambia: “Mwanamke, umefunguliwa kutoka kwa udhaifu wako.”+ 13 Yesu akaweka mikono juu ya yule mwanamke na mara moja akanyooka na kuanza kumtukuza Mungu. 14 Lakini ofisa msimamizi wa sinagogi akakasirika kwa sababu Yesu aliponya siku ya Sabato, akauambia umati: “Kuna siku sita za kufanya kazi;+ basi, njooni mponywe katika siku hizo, bali si siku ya Sabato.”+ 15 Hata hivyo, Bwana akajibu: “Wanafiki,+ je, kila mmoja wenu hamfungui ng’ombe au punda wake kutoka kwenye kibanda siku ya Sabato na kumpeleka akanywe maji?+ 16 Je, haifai kwa mwanamke huyu, binti ya Abrahamu, ambaye Shetani alikuwa amemfunga kwa miaka 18 afunguliwe kutoka kwenye kifungo hicho siku ya Sabato?” 17 Aliposema mambo hayo, wapinzani wake wote wakaanza kuaibika, lakini umati wote ukaanza kushangilia ulipoona mambo yenye utukufu aliyofanya.+
18 Basi akaendelea kusema: “Ufalme wa Mungu unafanana na nini, nitaulinganisha na nini? 19 Ni kama mbegu ya haradali ambayo mtu alichukua na kuipanda katika shamba lake, ikasitawi na kuwa mti, nao ndege wa angani wakajenga viota kwenye matawi yake.”+
20 Akauliza tena: “Nitaulinganisha Ufalme wa Mungu na nini? 21 Ni kama chachu* ambayo mwanamke alichukua na kuichanganya na vipimo* vitatu vikubwa vya unga mpaka unga wote ukachacha.”*+
22 Alipokuwa akisafiri kwenda Yerusalemu, Yesu alipita kutoka jiji mpaka jiji na kutoka kijiji mpaka kijiji akiwafundisha watu. 23 Sasa mtu fulani akamuuliza: “Bwana, je, wale watakaookolewa ni wachache?” Yesu akawaambia: 24 “Jitahidini sana ili mwingie kupitia mlango mwembamba,+ kwa sababu ninawaambia wengi watajaribu kuingia lakini hawataweza. 25 Mwenye nyumba atakaposimama na kuufunga mlango, mtakuwa nje mkibisha mlangoni, mkisema, ‘Bwana, tufungulie.’+ Lakini atawajibu: ‘Sijui mnatoka wapi.’ 26 Kisha mtamjibu, ‘Tulikula na kunywa pamoja nawe, nawe ulifundisha katika barabara zetu kuu.’+ 27 Lakini atawaambia, ‘Sijui mnatoka wapi. Ondokeni kwangu, ninyi nyote watenda maovu!’ 28 Hapo ndipo mtalia na kusaga meno yenu mtakapoona Abrahamu, Isaka, Yakobo, na manabii wote katika Ufalme wa Mungu, lakini ninyi mkiwa mmetupwa nje.+ 29 Isitoshe, watu watakuja kutoka mashariki na magharibi, na kutoka kaskazini na kusini, nao wataketi mezani katika Ufalme wa Mungu. 30 Tazama! kuna wale wa mwisho watakaokuwa wa kwanza, na kuna wale wa kwanza watakaokuwa wa mwisho.”+
31 Saa ileile baadhi ya Mafarisayo wakaja na kumwambia: “Ondoka hapa uende mahali pengine, kwa sababu Herode anataka kukuua.” 32 Akawaambia: “Nendeni mkamwambie mbweha huyo, ‘Tazama! Ninawafukuza roho waovu na kuwaponya watu leo na kesho, na siku ya tatu nitakuwa nimemaliza.’ 33 Hata hivyo, lazima niendelee leo, kesho, na keshokutwa, kwa sababu haiwezekani* nabii kuuawa nje ya Yerusalemu.+ 34 Yerusalemu, Yerusalemu, muuaji wa manabii na aliyewapiga mawe wale waliotumwa kwake+—nilijaribu mara ngapi kuwakusanya watoto wako, kama vile kuku anavyokusanya vifaranga wake chini ya mabawa yake! Lakini hamkutaka.+ 35 Tazama! Mmeachiwa nyumba yenu.+ Ninawaambia, hamtaniona tena mpaka mtakaposema, ‘Amebarikiwa yule anayekuja katika jina la Yehova!’”*+
14 Siku moja ya Sabato, Yesu alienda kula chakula katika nyumba ya kiongozi mmoja wa Mafarisayo, nao walikuwa wakimtazama sana. 2 Tazama! mbele yake kulikuwa na mtu mwenye ugonjwa wa kuvimba mwili.* 3 Basi Yesu akawauliza wale wenye ujuzi wa Sheria na Mafarisayo: “Je, ni halali au si halali kumponya mtu siku ya Sabato?”+ 4 Lakini wakanyamaza. Basi akamshika mtu huyo, akamponya na kumwambia aende zake. 5 Kisha akawauliza: “Ni nani kati yenu ambaye mwana wake au ng’ombe wake akianguka ndani ya kisima+ siku ya Sabato, hatamtoa humo mara moja?”+ 6 Wakashindwa kumjibu.
7 Kisha akawapa mfano watu walioalikwa, alipoona jinsi walivyokuwa wakichagua kuketi mahali pa heshima zaidi.+ Akawaambia: 8 “Mtu akikualika kwenye karamu ya ndoa, usiketi mahali pa heshima zaidi.+ Huenda pia amemwalika mtu mashuhuri kuliko wewe. 9 Naye aliyewaalika atakuja kukuambia, ‘Mwachie mtu huyu mahali ulipoketi.’ Kisha utaondoka kwa aibu na kuketi mahali pa chini kabisa. 10 Lakini unapoalikwa, nenda uketi mahali pa chini kabisa, ili mtu aliyekualika akija akuambie, ‘Rafiki yangu, nenda uketi mahali pa heshima zaidi.’ Kisha utakuwa na heshima mbele ya wageni wenzako wote.+ 11 Kwa maana kila mtu anayejiinua atanyenyekezwa, na yeyote anayejinyenyekeza atainuliwa.”+
12 Kisha akamwambia yule mtu aliyemwalika: “Unapoandaa mlo wa mchana au wa jioni, usiwaite rafiki zako, ndugu zako, watu wako wa ukoo, au jirani zako walio matajiri. Huenda wao pia wakakualika, na hivyo kukulipa ulichowafanyia. 13 Lakini unapoandaa karamu, waalike maskini, viwete, vilema, na vipofu;+ 14 nawe utakuwa mwenye furaha, kwa sababu hawana kitu cha kukulipa. Kwa maana utalipwa katika ufufuo+ wa waadilifu.”
15 Aliposikia mambo hayo, mmoja wa wageni akamwambia: “Mwenye furaha ni yule anayekula* katika Ufalme wa Mungu.”
16 Yesu akamwambia: “Mtu fulani alikuwa akiandaa mlo mkubwa wa jioni,+ naye akawaalika watu wengi. 17 Saa ya mlo wa jioni ilipofika, akamtuma mtumwa wake awaambie walioalikwa, ‘Njooni, kwa sababu kila kitu kiko tayari.’ 18 Lakini wote wakaanza kutoa visingizio.+ Mmoja akasema, ‘Nilinunua shamba, ninahitaji kwenda kuliona; tafadhali, niwie radhi.’ 19 Mwingine akasema, ‘Nimenunua jozi tano za ng’ombe,* ninaenda kuwakagua; tafadhali, niwie radhi.’+ 20 Na bado mwingine akasema, ‘Nimetoka tu kuoa, kwa hiyo siwezi kuja.’ 21 Basi yule mtumwa akarudi na kumwambia bwana wake mambo hayo. Kisha yule bwana wa nyumba akakasirika na kumwambia mtumwa wake, ‘Nenda upesi kwenye barabara kuu na vichochoro vya jiji, uwalete maskini, viwete, vipofu, na vilema.’ 22 Baada ya muda yule mtumwa akasema, ‘Bwana, nimefanya ulivyoniagiza, lakini bado kuna nafasi.’ 23 Basi yule bwana akamwambia mtumwa, ‘Nenda barabarani na kwenye vijia uwahimize watu waje, ili nyumba yangu ijae.+ 24 Kwa maana ninawaambia, hakuna hata mmoja wa watu waliokuwa wamealikwa atakayeonja mlo wangu wa jioni.’”+
25 Basi Yesu alikuwa akisafiri pamoja na umati mkubwa, kisha akageuka na kuwaambia: 26 “Yeyote akija kwangu naye hamchukii* baba yake na mama yake na mke wake na watoto wake na ndugu na dada zake, ndiyo, hata uhai wake*+ mwenyewe, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.+ 27 Yeyote asipouchukua mti wake wa mateso* na kunifuata hawezi kuwa mwanafunzi wangu.+ 28 Kwa mfano, ni nani kati yenu anayetaka kujenga mnara ambaye haketi kwanza na kuhesabu gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha? 29 La sivyo, ataweka msingi lakini ashindwe kumaliza, na wote wanaomtazama wataanza kumdhihaki, 30 wakisema: ‘Mtu huyu alianza kujenga lakini akashindwa kumaliza.’ 31 Au mfalme akienda kupigana vita na mfalme mwingine, je, haketi kwanza na kufikiri iwapo akiwa na wanajeshi 10,000 anaweza kumshinda yule anayekuja akiwa na wanajeshi 20,000? 32 Ikiwa hawezi, basi yule mfalme mwingine akiwa bado yuko mbali sana, yeye huwatuma mabalozi ili kufanya amani. 33 Vivyo hivyo, kwa hakika yeyote kati yenu asipoaga* mali zake zote hawezi kuwa mwanafunzi wangu.+
34 “Kwa kweli chumvi ni nzuri. Lakini ikipoteza nguvu yake, itakolezwa na nini?+ 35 Haifai kuchanganywa na udongo wala mbolea. Watu huitupa nje. Yule aliye na masikio ya kusikiliza na asikilize.”+
15 Basi wakusanya kodi wote na watenda dhambi walikuwa wakikusanyika karibu naye ili kumsikiliza.+ 2 Mafarisayo na waandishi wakaendelea kunung’unika wakisema: “Mtu huyu huwakaribisha watenda dhambi na kula pamoja nao.” 3 Ndipo akawaambia mfano huu: 4 “Ikiwa mmoja wenu ana kondoo 100, naye ampoteze mmoja, je, hatawaacha wale 99 nyikani aende kumtafuta yule aliyepotea mpaka ampate?+ 5 Na baada ya kumpata, anambeba mabegani na kushangilia. 6 Na anapofika nyumbani anawaita rafiki zake na jirani zake, na kuwaambia, ‘Shangilieni pamoja nami, kwa kuwa nimempata kondoo wangu aliyekuwa amepotea.’+ 7 Vivyo hivyo, ninawaambia kwamba kutakuwa na shangwe nyingi mbinguni kwa sababu ya mtenda dhambi mmoja anayetubu+ kuliko kwa waadilifu 99 ambao hawahitaji kutubu.
8 “Au mwanamke aliye na sarafu kumi za drakma* akipoteza drakma* moja, je, hatawasha taa, afagie nyumba yake na kuitafuta kwa makini mpaka aipate? 9 Na baada ya kuipata, anawaita rafiki zake* na jirani zake na kuwaambia, ‘Shangilieni pamoja nami, kwa kuwa nimeipata sarafu ya drakma* niliyokuwa nimepoteza.’ 10 Vivyo hivyo, ninawaambia kwamba malaika wa Mungu hushangilia mtenda dhambi mmoja anapotubu.”+
11 Kisha akasema: “Mtu fulani alikuwa na wana wawili. 12 Yule mdogo akamwambia baba yake, ‘Baba, nipe sehemu ya urithi ambayo ni yangu.’ Basi akawagawia wanawe mali yake. 13 Baada ya siku chache, yule mwana mdogo akakusanya vitu vyake vyote akasafiri kwenda nchi ya mbali, akiwa huko akatumia vibaya mali yake kwa kuishi maisha ya anasa.* 14 Alipokuwa ametumia kila kitu, njaa kali sana ikatokea katika nchi hiyo yote, naye hakuwa na chochote. 15 Hata alienda kuajiriwa na raia mmoja wa nchi hiyo, ambaye alimpeleka kwenye mashamba yake akalishe nguruwe.+ 16 Naye alitamani kujishibisha kwa maganda ya karuba ambayo nguruwe walikuwa wakila, lakini hakuna mtu aliyempa chochote.
17 “Aliporudiwa na fahamu akasema, ‘Baba yangu ameajiri wafanyakazi wengi nao wana mkate kwa wingi, lakini mimi ninakufa njaa! 18 Nitafunga safari kwenda kwa baba yangu na kumwambia: “Baba, nimetenda dhambi dhidi ya mbingu na dhidi yako. 19 Sistahili tena kuitwa mwanao. Naomba niwe mmoja wa wafanyakazi wako.”’ 20 Basi akaondoka na kwenda kwa baba yake. Akiwa mbali, baba yake akamwona na kumsikitikia, akakimbia, akamkumbatia* na kumbusu kwa wororo. 21 Kisha yule mwana akamwambia, ‘Baba, nimetenda dhambi dhidi ya mbingu na dhidi yako.+ Sistahili tena kuitwa mwanao.’ 22 Lakini baba yake akawaambia watumwa, ‘Leteni upesi kanzu bora zaidi na kumvika, pia mvisheni pete mkononi na viatu miguuni. 23 Vilevile, leteni ndama aliyenoneshwa, mchinjeni, nasi tule na tusherehekee, 24 kwa sababu huyu mwanangu alikuwa amekufa na sasa yuko hai;+ alikuwa amepotea naye amepatikana.’ Basi wakaanza kusherehekea.
25 “Sasa mwanawe mkubwa alikuwa shambani, alipokuwa akirudi na kukaribia nyumba, akasikia sauti ya muziki na dansi. 26 Basi akamwita mtumishi mmoja akamuuliza kilichokuwa kikiendelea. 27 Akamjibu, ‘Ndugu yako amerudi, kwa hiyo baba yako amechinja ndama aliyenoneshwa kwa sababu amerudi akiwa na afya njema.’* 28 Lakini akakasirika na kukataa kuingia ndani. Basi baba yake akatoka nje akaanza kumbembeleza. 29 Akamjibu baba yake, ‘Tazama! nimekutumikia kwa miaka mingi na sijawahi kuvunja amri yako hata mara moja, lakini hujawahi kunipa hata mara moja mwanambuzi ili nijifurahishe pamoja na rafiki zangu. 30 Lakini mara tu alipofika huyu mwanao aliyetumia vibaya* mali yako na makahaba, ulimchinjia ndama aliyenoneshwa.’ 31 Baba yake akamjibu, ‘Mwanangu, umekuwa pamoja nami sikuzote, na vitu vyangu vyote ni vyako. 32 Lakini ilibidi tusherehekee na kushangilia, kwa maana ndugu yako alikuwa amekufa lakini sasa yuko hai; alikuwa amepotea naye amepatikana.’”
16 Pia, Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Tajiri fulani alikuwa na msimamizi* ambaye alishtakiwa kwamba anatumia vibaya mali yake. 2 Basi akamwita na kumwambia, ‘Ni mambo gani haya ninayosikia kukuhusu? Lete rekodi za usimamizi kwa sababu huwezi tena kusimamia nyumba yangu.’ 3 Kisha yule msimamizi akajiambia, ‘Nitafanya nini kwa kuwa bwana wangu ananiondoa kazini? Sina nguvu za kulima na ninaona aibu kuombaomba. 4 Aha! Najua nitakachofanya, ili nitakapoachishwa kazi, watu wanikaribishe nyumbani mwao.’ 5 Akawaita mmoja mmoja wale waliokuwa na madeni ya bwana wake, akamuuliza wa kwanza, ‘Unadaiwa kiasi gani na bwana wangu?’ 6 Akajibu, ‘Vipimo* 100 vya mafuta ya zeituni.’ Akamwambia, ‘Chukua hati yako ya mapatano, uketi na upesi uandike 50.’ 7 Kisha akamuuliza mwingine, ‘Na wewe, unadaiwa kiasi gani?’ Akasema, ‘Vipimo vikubwa 100* vya ngano.’ Akamwambia, ‘Chukua hati yako ya mapatano uandike 80.’ 8 Bwana wake akamsifu yule msimamizi kwa sababu ingawa hakuwa mwadilifu, alitenda kwa hekima inayotumika;* kwa maana wana wa mfumo huu wa mambo* wana hekima zaidi katika kizazi chao kuliko walivyo wana wa nuru.+
9 “Pia, ninawaambia: Jifanyieni marafiki kupitia mali zisizo za uadilifu,+ ili zitakapokwisha wawapokee katika makao ya milele.+ 10 Mtu aliye mwaminifu katika lililo dogo ni mwaminifu katika lililo kubwa pia, na mtu asiye mwaminifu katika lililo dogo si mwaminifu katika lililo kubwa pia. 11 Kwa hiyo, msipokuwa waaminifu kuhusu mali zisizo za uadilifu, ni nani atakayewakabidhi kilicho cha kweli? 12 Na msipokuwa waaminifu kuhusu mali ya mtu mwingine, ni nani atakayewapa mali yenu wenyewe?+ 13 Hakuna mtumishi anayeweza kuwatumikia mabwana wawili, kwa maana atamchukia mmoja na kumpenda mwingine, au atashikamana na mmoja na kumdharau mwingine. Hamwezi kuwa watumwa wa Mungu na wa Utajiri.”+
14 Sasa Mafarisayo, waliopenda pesa, walikuwa wakisikiliza mambo hayo yote, nao wakaanza kumdhihaki.+ 15 Basi akawaambia: “Mnajitangaza kuwa waadilifu mbele ya wanadamu,+ lakini Mungu anaijua mioyo yenu.+ Kwa maana kitu kinachoheshimiwa sana na wanadamu kinamchukiza Mungu.+
16 “Sheria na Manabii walikuwa mpaka Yohana. Tangu wakati huo habari njema za Ufalme wa Mungu zinatangazwa, na watu wa namna zote wanajitahidi kuufikia.+ 17 Kwa kweli, ni rahisi zaidi kwa mbingu na dunia kupitilia mbali kuliko sehemu yoyote ya herufi ya Sheria kukosa kutimia.+
18 “Kila mtu anayempa talaka mke wake na kuoa mwingine anafanya uzinzi, na yeyote anayemwoa mwanamke aliyepewa talaka na mumewe anafanya uzinzi.+
19 “Kulikuwa na tajiri ambaye alikuwa akivaa mavazi ya zambarau na kitani, na alifurahia maisha ya kifahari siku kwa siku. 20 Lakini mtu fulani aliyekuwa akiombaomba aliyeitwa Lazaro, alikuwa akiletwa kwenye lango lake. Alikuwa na vidonda mwili mzima, 21 naye alikuwa akitamani kula mabaki yaliyoanguka kutoka kwenye meza ya yule tajiri. Ndiyo, pia, mbwa walikuwa wakija na kuramba vidonda vyake. 22 Baada ya muda yule mtu aliyekuwa akiombaomba akafa, malaika wakambeba na kumpeleka kando ya Abrahamu.*
“Pia, yule tajiri akafa na kuzikwa. 23 Akiwa Kaburini* akatazama juu, akiteseka sana, akamwona Abrahamu kwa mbali na Lazaro akiwa kando yake.* 24 Kwa hiyo akamwita, ‘Baba Abrahamu, nihurumie, umtume Lazaro achovye ncha ya kidole chake katika maji aupoze ulimi wangu, kwa maana ninateseka sana katika moto huu mkali.’ 25 Lakini Abrahamu akamwambia, ‘Mwanangu, kumbuka wewe ulikuwa na vitu vingi vizuri maishani, naye Lazaro aliteseka sana. Hata hivyo, sasa anafarijika lakini wewe unateseka. 26 Isitoshe, kuna shimo kubwa kati yetu nanyi, hivi kwamba wale wanaotaka kuvuka kutoka hapa kuja kwenu hawawezi, wala watu hawawezi kuvuka kutoka huko na kuja kwetu.’ 27 Kisha akasema, ‘Basi kama ni hivyo ninakuomba, baba, umtume kwenye nyumba ya baba yangu, 28 ili awatolee ushahidi kamili ndugu zangu watano wasije wakaingia mahali hapa pa mateso.’ 29 Lakini Abrahamu akasema, ‘Wana Musa na Manabii; waache wawasikilize hao.’+ 30 Kisha akasema, ‘Hapana, Baba Abrahamu, hawatasikiliza, lakini mtu fulani kutoka kwa wafu akienda kwao, watatubu.’ 31 Lakini akamwambia, ‘Kama hawamsikilizi Musa+ na Manabii, hawataamini hata mtu fulani akifufuliwa kutoka kwa wafu.’”
17 Ndipo akawaambia wanafunzi wake: “Lazima vikwazo vije. Hata hivyo, ole wake mtu atakayevisababisha! 2 Ingekuwa afadhali kwake kama angefungiwa shingoni jiwe la kusagia kisha atupwe baharini kuliko amkwaze mmoja wa hawa wadogo.+ 3 Jiangalieni ninyi wenyewe. Ndugu yako akitenda dhambi mkemee,+ na akitubu, msamehe.+ 4 Hata akikutendea dhambi mara saba kwa siku, naye anarudi kwako mara saba akisema, ‘ninatubu,’ unapaswa kumsamehe.”+
5 Mitume wakamwambia Bwana: “Tusaidie tuwe na imani zaidi.”+ 6 Bwana akasema: “Kama mngekuwa na imani inayolingana na mbegu ya haradali, mngeuambia mti huu wa mforsadi, ‘Ng’oka ukapandwe baharini!’ nao ungewatii.+
7 “Ni nani kati yenu aliye na mtumwa anayelima shamba au kuchunga wanyama, ambaye akirudi kutoka shambani, atamwambia ‘Njoo upesi, keti ule chakula’? 8 Hapana. Badala yake atamwambia, ‘Nitayarishie chakula cha jioni, na ujifunge vazi la kazi ili unihudumie mpaka nitakapomaliza kula na kunywa, kisha unaweza kula na kunywa.’ 9 Je, utamshukuru mtumwa huyo kwa sababu alifanya mambo uliyomwagiza? 10 Vivyo hivyo, baada ya kufanya mambo mliyoagizwa, semeni: ‘Sisi ni watumwa wasiofaa kitu. Tumefanya kile tulichopaswa kufanya.’”+
11 Alipokuwa akienda Yerusalemu, alipita kati ya Samaria na Galilaya. 12 Alipokuwa akiingia katika kijiji fulani alikutana na wanaume kumi wenye ukoma, lakini walisimama mbali naye.+ 13 Kisha wakasema kwa sauti kubwa: “Yesu, Mwalimu, tuhurumie!”* 14 Alipowaona, akawaambia: “Nendeni mkajionyeshe kwa makuhani.”+ Basi walipokuwa wakienda wakatakaswa.+ 15 Mmoja wao alipoona amepona, akarudi akimtukuza Mungu kwa sauti kubwa. 16 Akaanguka kifudifudi miguuni pa Yesu na kumshukuru. Isitoshe, alikuwa Msamaria.+ 17 Yesu akauliza: “Wote kumi walitakaswa, sivyo? Basi, wako wapi wale wengine tisa? 18 Je, hakuna mwingine aliyerudi ili kumtukuza Mungu isipokuwa mtu huyu wa taifa lingine?” 19 Kisha akamwambia: “Simama uende; imani yako imekuponya.”+
20 Mafarisayo walipomuuliza Ufalme wa Mungu utakuja lini,+ aliwajibu: “Ufalme wa Mungu hautakuja ukionekana waziwazi; 21 wala watu hawatasema, ‘Tazama! uko hapa!’ au, ‘Uko pale!’ Kwa maana tazama! Ufalme wa Mungu uko katikati yenu.”*+
22 Kisha akawaambia wanafunzi: “Siku zitafika ambapo mtatamani kuona moja kati ya siku za Mwana wa binadamu lakini hamtaiona. 23 Na watu watawaambia, ‘Angalia pale!’ au, ‘Angalia hapa!’ Msiende wala msiwafuate.+ 24 Kwa maana kama radi inavyong’aa kutoka sehemu moja ya mbingu mpaka sehemu nyingine, ndivyo Mwana wa binadamu+ atakavyokuwa katika siku yake.+ 25 Hata hivyo, kwanza lazima apatwe na mateso mengi na kukataliwa na kizazi hiki.+ 26 Isitoshe, kama ilivyokuwa katika siku za Noa,+ ndivyo itakavyokuwa katika siku za Mwana wa binadamu:+ 27 walikuwa wakila, walikuwa wakinywa, wanaume walikuwa wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina,+ na Gharika ikaja na kuwaangamiza wote.+ 28 Vivyo hivyo, kama ilivyokuwa katika siku za Loti:+ walikuwa wakila, walikuwa wakinywa, walikuwa wakinunua, walikuwa wakiuza, walikuwa wakipanda, na walikuwa wakijenga. 29 Lakini siku ambayo Loti alitoka Sodoma, kulinyesha mvua ya moto na kiberiti kutoka mbinguni na wote wakaangamizwa.+ 30 Ndivyo itakavyokuwa siku ambayo Mwana wa binadamu atafunuliwa.+
31 “Siku hiyo mtu aliye kwenye paa la nyumba asishuke kuchukua mali iliyo ndani ya nyumba yake, vivyo hivyo mtu aliye shambani, asirudi kwenye vitu vilivyo nyuma. 32 Mkumbukeni mke wa Loti.+ 33 Yeyote anayetaka kuuokoa uhai wake* ataupoteza, lakini yeyote anayeupoteza atauokoa.+ 34 Ninawaambia, usiku huo watu wawili watakuwa katika kitanda kimoja; mmoja atachukuliwa, lakini mwingine ataachwa.+ 35 Wanawake wawili watakuwa wakisaga kwenye jiwe moja la kusagia; mmoja atachukuliwa na mwingine ataachwa.” 36* —— 37 Basi wakamuuliza: “Wapi, Bwana?” Akawajibu: “Mahali palipo na mzoga, hapo ndipo tai watakapokusanyika.”+
18 Kisha akawaambia mfano ili kuwaonyesha umuhimu wa kuendelea kusali bila kukata tamaa.+ 2 Akasema: “Katika jiji fulani kulikuwa na mwamuzi ambaye hakumwogopa Mungu wala hakumheshimu mtu yeyote. 3 Pia, katika jiji hilo kulikuwa na mjane ambaye alikuwa akienda kwake na kumwomba, ‘Hakikisha kwamba kesi yangu itaamuliwa kwa haki.’ 4 Kwa muda fulani yule mwamuzi alikataa, lakini baadaye akajiambia, ‘Ingawa simwogopi Mungu wala simheshimu mtu yeyote, 5 kwa sababu huyu mjane anaendelea kunisumbua, nitahakikisha amepata haki ili asiendelee kuja kunichosha na maombi yake.’”*+ 6 Kisha Bwana akasema: “Sikieni alichosema mwamuzi huyo ingawa si mwadilifu! 7 Kwa hakika, je, Mungu hatawatendea haki watu wake waliochaguliwa ambao wanamlilia mchana na usiku,+ huku akiwaonyesha subira?+ 8 Ninawaambia, atawatendea haki upesi. Hata hivyo, Mwana wa binadamu atakapofika, je, kweli ataipata imani hii* duniani?”
9 Pia, aliwaambia mfano huu wale waliojiona kuwa waadilifu na kuwadharau wengine: 10 “Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali, mmoja alikuwa Farisayo na mwingine mkusanya kodi. 11 Yule Farisayo akasimama na kuanza kusali akisema moyoni, ‘Ee Mungu, ninakushukuru kwa sababu mimi si kama watu wengine—wanyang’anyi, wasio waadilifu, wazinzi—au hata kama mkusanya kodi huyu. 12 Mimi hufunga mara mbili kwa juma; ninatoa sehemu ya kumi ya mapato yangu yote.’+ 13 Lakini yule mkusanya kodi alikuwa amesimama mbali kidogo na hata hakutaka kutazama mbinguni, bali alijipigapiga kifuani akisema, ‘Ee Mungu, nihurumie* mimi mtenda dhambi.’+ 14 Ninawaambia, mtu huyu alishuka kwenda nyumbani akiwa mwadilifu mbele za Mungu kuliko yule Farisayo.+ Kwa sababu kila mtu anayejiinua atafedheheshwa, lakini yeyote anayejinyenyekeza atainuliwa.”+
15 Sasa watu wakamletea Yesu watoto wao wadogo ili awaguse, lakini wanafunzi walipoona hivyo wakaanza kuwakemea.+ 16 Lakini Yesu akawaita wale watoto, akisema: “Waacheni watoto wadogo waje kwangu, na msijaribu kuwazuia, kwa maana Ufalme wa Mungu ni wa wale walio kama wao.+ 17 Kwa kweli ninawaambia, yeyote asiyeupokea Ufalme wa Mungu kama mtoto mdogo hataingia kamwe ndani yake.”+
18 Mtawala fulani akamuuliza: “Mwalimu Mwema, ninapaswa kufanya nini ili niurithi uzima wa milele?”+ 19 Yesu akamwambia: “Kwa nini unaniita mwema? Hakuna aliye mwema, isipokuwa mmoja, Mungu.+ 20 Unazijua amri hizi: ‘Usifanye uzinzi,+ usiue,+ usiibe,+ usitoe ushahidi wa uwongo,+ mheshimu baba yako na mama yako.’”+ 21 Ndipo akasema: “Nimeyashika hayo yote tangu nilipokuwa kijana.” 22 Baada ya kusikia hilo, Yesu akamwambia, “Bado kuna jambo unalokosa: Uza kila kitu ulicho nacho na uwagawie maskini pesa hizo, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha uje uwe mfuasi wangu.”+ 23 Aliposikia hivyo, akahuzunika sana, kwa sababu alikuwa tajiri sana.+
24 Yesu akamtazama na kusema: “Itakuwa vigumu sana kwa wale walio na pesa kuingia katika Ufalme wa Mungu!+ 25 Kwa kweli, ni rahisi zaidi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano ya kushonea kuliko tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu.”+ 26 Wale waliosikia hilo wakauliza: “Ni nani anayeweza kuokolewa?”+ 27 Akasema: “Mambo yasiyowezekana kwa wanadamu yanawezekana kwa Mungu.”+ 28 Lakini Petro akamwambia: “Tazama! Tumeacha vitu vyetu na kukufuata.”+ 29 Akawaambia: “Kwa kweli ninawaambia, hakuna yeyote ambaye ameacha nyumba, au mke, au ndugu, au wazazi, au watoto kwa ajili ya Ufalme wa Mungu+ 30 ambaye hatapata mara nyingi zaidi wakati huu, na katika mfumo wa mambo* unaokuja, uzima wa milele.”+
31 Ndipo akawaita kando wale 12 na kuwaambia: “Tazama! Tunapanda kwenda Yerusalemu, na mambo yote yaliyoandikwa kupitia manabii kuhusu Mwana wa binadamu yatatimia.*+ 32 Kwa mfano, atatiwa mikononi mwa watu wa mataifa+ naye atadhihakiwa,+ atatendewa kwa dharau, na kutemewa mate.+ 33 Watampiga mijeledi, kisha watamuua,+ lakini siku ya tatu atafufuka.”+ 34 Hata hivyo, hawakuelewa maana ya mambo hayo, kwa sababu walikuwa wamefichwa maneno hayo, nao hawakuelewa mambo yaliyosemwa.
35 Yesu alipokaribia Yeriko kipofu mmoja alikuwa ameketi kando ya barabara akiombaomba.+ 36 Aliposikia umati ukipita, akaanza kuuliza kilichokuwa kikiendelea. 37 Wakamjibu: “Yesu Mnazareti ndiye anayepita!” 38 Ndipo akasema kwa sauti kubwa: “Yesu, Mwana wa Daudi, nihurumie!”* 39 Wale waliokuwa mbele wakaanza kumkemea wakimwambia anyamaze, lakini akazidi kusema kwa sauti kubwa: “Mwana wa Daudi, nihurumie!”* 40 Kisha Yesu akasimama na kuagiza mtu huyo aletwe kwake. Alipokaribia, Yesu akamuuliza: 41 “Unataka nikufanyie nini?” Akasema: “Bwana, naomba niweze kuona tena.” 42 Basi Yesu akamwambia: “Ona tena; imani yako imekuponya.”+ 43 Mara moja akaanza kuona tena, naye akaanza kumfuata Yesu+ huku akimtukuza Mungu. Pia, watu wote walipoona hayo, wakamsifu Mungu.+
19 Yesu akaingia Yeriko, naye alikuwa akipita katika jiji hilo. 2 Kulikuwa na mwanamume aliyeitwa Zakayo; alikuwa mkuu wa wakusanya kodi, na alikuwa tajiri. 3 Basi, alitamani sana kumwona Yesu, lakini hakuweza kwa sababu ya umati, kwa maana alikuwa mfupi. 4 Basi akakimbia mbele na kupanda juu ya mti wa mkuyu* ili amwone Yesu, kwa maana alikuwa karibu kupitia njia hiyo. 5 Yesu alipofika hapo, akatazama juu akamwambia: “Zakayo, shuka haraka, kwa maana leo lazima nikae nyumbani kwako.” 6 Basi akashuka haraka na kumkaribisha kwa shangwe awe mgeni wake. 7 Wote walipoona hivyo, wakaanza kunung’unika wakisema: “Ameenda kumtembelea mtenda dhambi.”+ 8 Lakini Zakayo akasimama na kumwambia Bwana: “Tazama! Nitawapa maskini nusu ya mali zangu, Bwana, na chochote nilichomnyang’anya mtu,* nitamrudishia mara nne.”+ 9 Ndipo Yesu akamwambia: “Leo wokovu umekuja katika nyumba hii, kwa sababu yeye pia ni mwana wa Abrahamu. 10 Kwa maana Mwana wa binadamu alikuja kutafuta na kuokoa kilichopotea.”+
11 Walipokuwa wakisikiliza mambo hayo, akawaambia mfano mwingine, kwa sababu alikuwa karibu na Yerusalemu nao walifikiri Ufalme wa Mungu ungetokea ghafla.+ 12 Basi akasema: “Mtu fulani wa familia mashuhuri alitaka kusafiri kwenda nchi ya mbali+ ili apokee mamlaka ya kifalme kisha arudi. 13 Akawaita kumi kati ya watumwa wake akawapa mina* kumi na kuwaambia, ‘Fanyeni nazo biashara mpaka nitakaporudi.’+ 14 Lakini raia zake walimchukia, nao wakatuma mabalozi wamfuate na kusema, ‘Hatutaki mtu huyu awe mfalme wetu.’
15 “Mwishowe aliporudi baada ya kupokea mamlaka ya kifalme,* aliwaita watumwa aliokuwa amewapa pesa,* ili ajue faida waliyopata kwa kufanya biashara.+ 16 Basi wa kwanza akaja na kusema, ‘Bwana, mina yako moja imeleta faida ya mina kumi.’+ 17 Akamwambia, ‘Umefanya vema, mtumwa mwema! Kwa kuwa umekuwa mwaminifu katika jambo dogo sana, utatawala majiji kumi.’+ 18 Kisha wa pili akaja na kusema, ‘Bwana, mina yako moja, imeleta faida ya mina tano.’+ 19 Vilevile akamwambia, ‘Wewe pia, utatawala majiji matano.’ 20 Lakini mwingine akaja, akasema, ‘Bwana, hii hapa mina yako, niliifunga kwa kitambaa nikaificha. 21 Nilikuogopa kwa sababu wewe ni mtu mkali; wewe huchukua kile ambacho hukuweka akiba, na kuvuna kile ambacho hukupanda.’+ 22 Akamwambia, ‘Ninakuhukumu kwa maneno yako mwenyewe, mtumwa mwovu. Ulijua, sivyo, kwamba mimi ni mtu mkali, ambaye huchukua kile ambacho sikuweka akiba na kuvuna kile ambacho sikupanda?+ 23 Basi kwa nini hukuziweka pesa* zangu benki? Kisha baada ya kurudi, ningezichukua zikiwa na faida.’
24 “Ndipo akawaambia wale waliokuwa wamesimama hapo, ‘Chukueni mina hiyo mkampe yule aliye na mina kumi.’+ 25 Lakini wakamwambia, ‘Bwana, tayari huyo ana mina kumi!’— 26 ‘Ninawaambia, kila mtu aliye na kitu, ataongezewa, lakini yule asiye na kitu, hata kile alicho nacho kitachukuliwa.+ 27 Isitoshe, waleteni adui zangu ambao hawakutaka niwe mfalme wao, muwaue mbele yangu.’”
28 Baada ya Yesu kusema hayo, akapanda kuelekea Yerusalemu. 29 Alipokaribia Bethfage na Bethania kwenye Mlima wa Mizeituni,+ akawatuma wawili kati ya wanafunzi,+ 30 akisema: Nendeni katika kijiji mtakachokiona, na mtakapoingia mtamwona mwanapunda akiwa amefungwa, ambaye hakuna mtu amewahi kuketi juu yake. Mfungueni na kumleta. 31 Lakini mtu akiwauliza, ‘Kwa nini mnamfungua?’ Mwambieni, ‘Bwana anamhitaji.’” 32 Basi wale waliotumwa wakaenda na kupata sawasawa na vile Yesu alivyowaambia.+ 33 Lakini walipokuwa wakimfungua mwanapunda huyo, wenyewe wakawauliza: “Mbona mnamfungua huyo mwanapunda?” 34 Wakajibu: “Bwana anamhitaji.” 35 Wakampeleka kwa Yesu, nao wakaweka mavazi yao ya nje juu ya huyo mwanapunda na kumketisha Yesu juu yake.+
36 Alipokuwa akienda walikuwa wakitandaza mavazi yao ya nje barabarani.+ 37 Alipokaribia tu barabara ya kushuka Mlima wa Mizeituni umati wote wa wanafunzi ukaanza kushangilia na kumsifu Mungu kwa sauti kubwa kwa sababu ya matendo yote yenye nguvu ambayo walikuwa wameona, 38 na kusema: “Amebarikiwa yule anayekuja akiwa Mfalme katika jina la Yehova!* Amani mbinguni, na utukufu katika vilele vilivyo juu!”+ 39 Hata hivyo, baadhi ya Mafarisayo waliokuwa kwenye umati wakamwambia: “Mwalimu, wakemee wanafunzi wako.”+ 40 Lakini akajibu: “Ninawaambia, hata hawa wakinyamaza, mawe yatapaza sauti.”
41 Alipokaribia jiji la Yerusalemu, akalitazama na kulililia,+ 42 akisema: “Kama wewe, naam wewe, ungefahamu leo mambo yanayokuletea amani—lakini sasa yamefichwa kutoka machoni pako.+ 43 Kwa sababu siku zitakuja, adui zako watakapojenga ngome yenye miti iliyochongoka kukuzunguka, nao watakuzingira* kila upande.+ 44 Watakuangusha chini wewe na watoto wako walio ndani yako,+ nao hawataacha jiwe juu ya jiwe lingine,+ kwa sababu hukutambua wakati wa kukaguliwa kwako.”
45 Kisha akaingia hekaluni na kuanza kuwafukuza wale waliokuwa wakiuza,+ 46 akiwaambia: “Imeandikwa, ‘Nyumba yangu itakuwa nyumba ya sala,’+ lakini mmeifanya kuwa pango la wanyang’anyi.”+
47 Akaendelea kufundisha kila siku hekaluni. Lakini wakuu wa makuhani, waandishi na viongozi wa watu walikuwa wakitaka kumuua;+ 48 hata hivyo hawakufanikiwa, kwa maana watu wote walikuwa wakimfuata sana ili wamsikilize.+
20 Siku moja alipokuwa akifundisha watu hekaluni na kutangaza habari njema, wakuu wa makuhani, waandishi na wazee wakaja, 2 nao wakasema: “Tuambie, unafanya mambo haya kwa mamlaka gani? Au ni nani aliyekupa mamlaka hayo?”+ 3 Akawajibu: “Mimi pia nitawauliza swali, nanyi mnijibu: 4 Je, ubatizo wa Yohana ulitoka mbinguni au kwa wanadamu?”* 5 Wakaanza kujadiliana kati yao wakisema: “Tukisema, ‘Ulitoka mbinguni,’ atatuuliza, ‘Kwa nini hamkumwamini?’ 6 Lakini tukisema, ‘Ulitoka kwa wanadamu,’ watu wote watatupiga mawe, kwa sababu wanaamini Yohana alikuwa nabii.”+ 7 Basi wakamjibu kwamba hawajui chanzo chake. 8 Yesu akawaambia: “Nami siwaambii ninafanya mambo haya kwa mamlaka gani.”
9 Yesu akaanza kuwaambia watu mfano huu: “Mtu fulani alipanda shamba la mizabibu+ akalikodisha kwa wakulima, kisha akasafiri kwenda ng’ambo, akakaa huko muda mrefu.+ 10 Majira yalipofika akamtuma mtumwa kwa wakulima ili wampe baadhi ya matunda ya shamba la mizabibu. Hata hivyo, wale wakulima wakampiga na kumfukuza mikono mitupu.+ 11 Lakini akamtuma mtumwa mwingine. Huyo pia wakampiga, wakamwaibisha,* na kumfukuza mikono mitupu. 12 Bado tena akamtuma wa tatu; huyo pia walimjeruhi na kumtupa nje. 13 Ndipo mwenye shamba la mizabibu akasema, ‘Nifanye nini? Nitamtuma mwanangu mpendwa.+ Labda watamheshimu.’ 14 Wakulima walipomwona wakaambiana, ‘Huyu ndiye mrithi. Basi tumuue, ili urithi wake uwe wetu.’ 15 Wakamtupa nje ya shamba la mizabibu na kumuua.+ Kwa hiyo, mwenye shamba la mizabibu atawafanya nini? 16 Atakuja na kuwaua wakulima hao, kisha atawapa watu wengine shamba hilo la mizabibu.”
Waliposikia hivyo wakasema: “Jambo hilo lisitukie kamwe!” 17 Lakini akawatazama moja kwa moja na kusema: “Basi, andiko hili linamaanisha nini: ‘Jiwe ambalo wajenzi walilikataa, limekuwa jiwe kuu la pembeni’?*+ 18 Kila mtu anayeanguka kwenye jiwe hilo atavunjika vipandevipande.+ Na litamponda yeyote litakayemwangukia.”
19 Waandishi na wakuu wa makuhani walitambua kwamba mfano aliosema uliwahusu, basi walitaka kumkamata saa hiyo hiyo, lakini waliwaogopa watu.+ 20 Baada ya kumtazama kwa makini, wakatuma watu waliowakodi kisiri wajifanye kuwa waadilifu ili wamnase Yesu kwa maneno yake+ na kumkabidhi kwa serikali na kwa mamlaka ya gavana. 21 Nao wakamuuliza: “Mwalimu, tunajua wewe husema na kufundisha kwa usahihi na huna ubaguzi, bali unafundisha njia ya Mungu kupatana na kweli: 22 Je, ni halali* au si halali kwetu kumlipa Kaisari kodi?”* 23 Lakini alitambua ujanja wao na kuwaambia: 24 “Nionyesheni dinari.* Ina sura na maandishi ya nani?” Wakajibu: “Kaisari.” 25 Akawaambia: “Basi mlipeni Kaisari+ vitu vya Kaisari, na Mungu vitu vya Mungu.”+ 26 Kwa hiyo, wakashindwa kumnasa kwa maneno yake mbele ya watu, nao wakanyamaza wakiwa wameshangazwa na jibu lake.
27 Hata hivyo, baadhi ya Masadukayo, ambao husema hakuna ufufuo,+ wakaja na kumuuliza:+ 28 “Mwalimu, Musa alituandikia, ‘Ndugu ya mtu akifa na kumwacha mke, lakini hakuwa na mtoto, ndugu yake anapaswa kumchukua mke huyo ili kumwinulia ndugu yake uzao.’+ 29 Basi kulikuwa na ndugu saba. Wa kwanza alioa mwanamke lakini akafa bila mtoto. 30 Na wa pili 31 na wa tatu, wakamwoa mwanamke huyo. Vivyo hivyo wote saba; walikufa bila kupata watoto. 32 Mwishowe pia yule mwanamke akafa. 33 Kwa hiyo, katika ufufuo, atakuwa mke wa nani? Kwa maana wote saba walikuwa wamemwoa.”
34 Yesu akawaambia: “Watoto wa mfumo huu wa mambo* huoa na kuolewa, 35 lakini wale waliohesabiwa kuwa wanastahili kuupata mfumo huo wa mambo na kufufuliwa kutoka kwa wafu hawaoi wala kuolewa.+ 36 Kwa kweli, hawawezi kufa tena kamwe, kwa maana wao ni kama malaika, nao ni watoto wa Mungu kwa kuwa watoto wa ufufuo. 37 Lakini hata Musa alifunua kwamba wafu watafufuliwa, katika masimulizi kuhusu kichaka cha miiba, anapomwita Yehova* ‘Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo.’+ 38 Yeye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai, kwa maana kwake,* wote wako hai.”+ 39 Baadhi ya waandishi wakasema: “Mwalimu, umesema vema.” 40 Kwa maana hawakuwa tena na ujasiri wa kumuuliza hata swali moja.
41 Naye akawauliza: “Kwa nini watu husema kwamba Kristo ni mwana wa Daudi?+ 42 Kwa maana Daudi mwenyewe anasema katika kitabu cha Zaburi, ‘Yehova* alimwambia Bwana wangu: “Keti kwenye mkono wangu wa kuume 43 mpaka niwaweke maadui wako kuwa kiti cha miguu yako.”’+ 44 Basi, Daudi anamwita Bwana; kwa hiyo anawezaje kuwa mwanawe?”
45 Watu wote walipokuwa wakimsikiliza, akawaambia wanafunzi wake: 46 “Jihadharini na waandishi wanaopenda kutembea wakiwa wamevaa kanzu na wanaopenda kusalimiwa sokoni, na viti vya mbele* katika masinagogi na mahali penye heshima zaidi kwenye milo ya jioni,+ 47 na ambao humaliza nyumba* za wajane na kutoa sala ndefu ili waonekane.* Hao watapata hukumu kali* zaidi.”
21 Yesu alipotazama, aliwaona matajiri wakitumbukiza zawadi zao katika masanduku* ya hazina.+ 2 Ndipo akamwona mjane mmoja maskini akitumbukiza sarafu mbili ndogo zenye thamani ndogo sana,*+ 3 naye akasema: “Kwa kweli ninawaambia, mjane huyu maskini ametumbukiza zaidi ya wote.+ 4 Kwa maana wote hao walitumbukiza zawadi kutokana na ziada yao, lakini mwanamke huyu ingawa ni maskini* alitumbukiza riziki yake yote.”+
5 Baadaye, watu fulani walipokuwa wakisema jinsi hekalu lilivyopambwa kwa mawe mazuri na vitu vilivyowekwa wakfu,+ 6 akawaambia: “Vitu hivi mnavyoona, siku zitakuja ambapo hakuna jiwe litakaloachwa juu ya jiwe lingine bila kuangushwa chini.”+ 7 Ndipo wakamuuliza: “Mwalimu, kwa kweli mambo haya yatatukia lini, na ni ishara gani itakayoonyesha kwamba mambo haya yanakaribia kutokea?”+ 8 Akasema: “Jihadharini msipotoshwe,+ kwa maana wengi watakuja kwa msingi wa jina langu, wakisema, ‘Mimi ndiye,’ na, ‘Wakati unaofaa umekaribia.’ Msiwafuate.+ 9 Pia, mtakaposikia kuhusu vita na machafuko* msiogope. Kwa maana lazima mambo hayo yatukie kwanza, lakini ule mwisho hautatokea mara moja.”+
10 Kisha akawaambia: “Taifa litapigana na taifa,+ na ufalme kupigana na ufalme.+ 11 Kutakuwa na matetemeko makubwa ya ardhi, na magonjwa na upungufu wa chakula katika sehemu mbalimbali;+ pia kutakuwa na mambo yenye kuogopesha na ishara kubwa kutoka mbinguni.
12 “Lakini kabla ya mambo hayo yote kutokea, watu watawakamata ninyi na kuwatesa+ na kuwakabidhi kwenye masinagogi na magereza. Mtapelekwa mbele ya wafalme na magavana kwa sababu ya jina langu.+ 13 Hivyo, mtapata nafasi ya kutoa ushahidi. 14 Kwa hiyo, azimieni mioyoni mwenu kwamba hamtafanya mazoezi mapema kuhusu jinsi mtakavyojitetea,+ 15 kwa maana nitawapa maneno na hekima, ambayo wapinzani wenu wote kwa pamoja hawataweza kushindana nayo wala kubisha.+ 16 Zaidi ya hayo, mtakabidhiwa* hata na wazazi, ndugu, watu wa ukoo, na rafiki zenu, nao watawaua baadhi yenu,+ 17 nanyi mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu.+ 18 Lakini hakuna hata unywele mmoja wa vichwa vyenu utakaoangamia.+ 19 Mkivumilia, mtauokoa uhai wenu.*+
20 “Hata hivyo, mtakapoona Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi,+ jueni kwamba linakaribia kuharibiwa.+ 21 Ndipo wale walio Yudea waanze kukimbilia milimani,+ na wale walio Yerusalemu waondoke, nao wale walio mashambani wasiingie ndani yake, 22 kwa sababu hizi ni siku za kutekeleza haki,* ili mambo yote yaliyoandikwa yatimizwe. 23 Ole wao wanawake wenye mimba na wale wanaonyonyesha mtoto katika siku hizo!+ Kwa maana kutakuwa na mateso mengi katika nchi na ghadhabu dhidi ya watu hawa. 24 Nao wataangamizwa kwa upanga na watapelekwa utekwani katika mataifa yote;+ na Yerusalemu litakanyagwa-kanyagwa na mataifa,* mpaka nyakati zilizowekwa za mataifa* zitimie.+
25 “Pia, kutakuwa na ishara katika jua na mwezi na nyota,+ na duniani mataifa yatakuwa na maumivu makali bila kujua cha kufanya kwa sababu ya mngurumo na msukosuko wa bahari. 26 Watu watazimia kwa woga wakitarajia mambo yatakayotokea juu ya dunia inayokaliwa, kwa maana nguvu za mbingu zitatikiswa. 27 Ndipo watakapomwona Mwana wa binadamu+ akija katika mawingu akiwa na nguvu na utukufu mwingi.+ 28 Lakini mambo hayo yatakapoanza kutukia, simameni wima na kuinua vichwa vyenu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia.”
29 Ndipo akawaambia mfano huu: “Angalieni mtini na miti mingine yote.+ 30 Inapochipua, mnaona na kujua kwamba kiangazi kinakaribia. 31 Vivyo hivyo, ninyi pia mtakapoona mambo hayo yakitukia, jueni kwamba Ufalme wa Mungu umekaribia. 32 Kwa kweli ninawaambia, kizazi hiki hakitapitilia mbali kamwe mpaka mambo yote yatukie.+ 33 Mbingu na dunia zitapitilia mbali, lakini maneno yangu hayatapitilia mbali kamwe.+
34 “Lakini jiangalieni wenyewe ili mioyo yenu isilemewe kamwe na kula na kunywa kupita kiasi+ na mahangaiko ya maisha,+ na siku ile iwakute ghafla 35 kama mtego.+ Kwa maana itakuja juu ya wale wote wanaoishi juu ya uso wa dunia. 36 Basi, endeleeni kukesha+ sikuzote mkiomba dua+ ili mfanikiwe kuponyoka mambo yote hayo ambayo lazima yatukie, na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.”+
37 Yesu alikuwa akifundisha hekaluni mchana, lakini usiku alienda kukaa kwenye Mlima wa Mizeituni. 38 Watu wote walikuwa wakija hekaluni asubuhi na mapema ili wamsikilize.
22 Sasa Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu, inayoitwa, Pasaka,+ ilikuwa imekaribia.+ 2 Nao wakuu wa makuhani na waandishi walikuwa wakitafuta njia bora ya kumuua,+ kwa sababu waliwaogopa watu.+ 3 Ndipo Shetani akamwingia Yuda, aliyeitwa Iskariote, ambaye alikuwa mmoja wa wale 12,+ 4 naye akaenda kuongea na wakuu wa makuhani na makapteni wa hekalu kuhusu jinsi atakavyomsaliti kwao.+ 5 Wakafurahishwa na jambo hilo, nao wakakubaliana kumpa fedha.+ 6 Basi akakubali na kuanza kutafuta nafasi nzuri ya kumsaliti kwao bila umati kuwapo.
7 Siku ya Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu ikafika, siku ambayo dhabihu ya Pasaka hutolewa;+ 8 basi Yesu akawatuma Petro na Yohana, akawaambia: “Nendeni mkatutayarishie Pasaka tule.”+ 9 Wakamuuliza: “Unataka tuitayarishe wapi?” 10 Akawaambia: “Tazameni! Mtakapoingia jijini, mtakutana na mwanamume akiwa amebeba mtungi wa maji. Mfuateni mwingie katika nyumba atakayoingia.+ 11 Mwambieni mwenye nyumba hiyo, ‘Mwalimu anasema: “Kiko wapi chumba cha wageni ambamo ninaweza kula Pasaka pamoja na wanafunzi wangu?”’ 12 Mtu huyo atawaonyesha chumba kikubwa cha juu chenye vifaa. Tayarisheni humo.” 13 Basi wakaenda na kupata kama alivyokuwa amewaambia, nao wakaandaa Pasaka.
14 Wakati ulipofika, akaketi mezani pamoja na mitume.+ 15 Akawaambia: “Nimetamani sana kula Pasaka hii pamoja nanyi kabla sijateseka; 16 kwa maana ninawaambia, sitakula tena Pasaka mpaka itakapotimizwa katika Ufalme wa Mungu.” 17 Yesu akapokea kikombe, akashukuru na kusema: “Chukueni kikombe hiki na mkipitishe kutoka kwa mmoja mpaka kwa mwingine kati yenu, 18 kwa maana ninawaambia, kuanzia sasa sitakunywa tena divai ya mzabibu mpaka Ufalme wa Mungu utakapokuja.”
19 Pia, akachukua mkate,+ akashukuru na kuumega, akawapa akisema: “Huu unamaanisha mwili wangu,+ ambao utatolewa kwa ajili yenu.+ Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka.”+ 20 Pia, akafanya vivyo hivyo na kile kikombe baada ya wao kula mlo wa jioni, akisema: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya+ kwa msingi wa damu yangu,+ ambayo itamwagwa kwa ajili yenu.+
21 “Lakini tazameni! mkono wa msaliti wangu uko pamoja nami mezani.+ 22 Kwa kweli, Mwana wa binadamu anaenda zake kama ilivyotabiriwa;+ lakini ole wake mtu atakayemsaliti!”+ 23 Kwa hiyo wakaanza kuulizana ni nani kati yao ambaye angemsaliti.+
24 Hata hivyo, pia kukatokea bishano kali kuhusu ni nani aliyekuwa mkuu zaidi kati yao.+ 25 Lakini akawaambia: “Wafalme wa mataifa hupiga ubwana juu yao, na wale walio na mamlaka juu yao huitwa Wafadhili.+ 26 Hata hivyo, ninyi hampaswi kuwa hivyo.+ Lakini yule aliye mkuu zaidi kati yenu anapaswa kuwa mdogo zaidi,+ na yule anayeongoza awe kama anayehudumu. 27 Kwa maana ni nani aliye mkuu zaidi, yule anayekula* au yule anayehudumu?* Ni yule anayekula,* sivyo? Lakini mimi ni kama mtu anayehudumu* kati yenu.+
28 “Hata hivyo, ninyi ndio mmeshikamana nami+ katika majaribu yangu;+ 29 nami ninafanya agano pamoja nanyi, kama Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme,+ 30 ili mle na kunywa mezani pangu katika Ufalme wangu,+ na kuketi kwenye viti vya ufalme+ ili kuyahukumu makabila 12 ya Israeli.+
31 “Simoni, Simoni, tazama! Shetani anataka kuwapata ninyi nyote ili awapepete kama ngano.+ 32 Lakini nimeomba dua kwa ajili yako ili imani yako isidhoofike;+ nawe utakaporudi, watie nguvu ndugu zako.”+ 33 Petro akasema: “Bwana, niko tayari kwenda nawe gerezani na hata kufa nawe.”+ 34 Lakini akamwambia: “Petro ninakuambia, leo kabla jogoo hajawika utanikana mara tatu.”+
35 Akawauliza: “Nilipowatuma bila mkoba wa pesa, mfuko wa chakula, na viatu,+ je, mlikosa chochote?” Wakajibu: “Hapana!” 36 Kisha akawaambia: “Lakini sasa yule aliye na mkoba wa pesa au mfuko wa chakula aubebe, na yule asiye na upanga, auze vazi lake la nje anunue upanga. 37 Kwa maana ninawaambia mambo yaliyoandikwa kunihusu yatatimia, yaani, ‘Naye alihesabiwa pamoja na waasi sheria.’+ Kwa maana hilo linatimia kunihusu.”+ 38 Kisha wakasema: “Bwana, tazama! hapa pana panga mbili.” Akawaambia: “Inatosha.”
39 Alipoondoka, kama kawaida yake alienda kwenye Mlima wa Mizeituni, nao wanafunzi pia wakamfuata.+ 40 Walipofika huko akawaambia: “Endeleeni kusali ili msiingie katika majaribu.”+ 41 Akawaacha na kwenda umbali wa mtupo wa jiwe, akapiga magoti na kuanza kusali, 42 akisema: “Baba, ukipenda, niondolee kikombe hiki. Hata hivyo, si kama ninavyopenda, bali mapenzi yako na yatendeke.”+ 43 Ndipo malaika kutoka mbinguni akaja na kumtia nguvu.+ 44 Lakini alikuwa na maumivu makali hivi kwamba akaendelea kusali kwa bidii zaidi;+ na jasho lake likawa kama matone ya damu yakidondoka chini. 45 Baada ya kusali, akawaendea wanafunzi, akawakuta wakiwa wamelala usingizi, wakiwa wamechoka kwa sababu ya huzuni.+ 46 Akawaambia: “Kwa nini mnalala? Amkeni mwendelee kusali, ili msiingie katika majaribu.”+
47 Alipokuwa bado akizungumza, tazama! umati ukaja ukiongozwa na Yuda, mmoja wa wale 12, naye akamkaribia Yesu ili ambusu.+ 48 Lakini Yesu akamuuliza: “Yuda, unamsaliti Mwana wa binadamu kwa busu?” 49 Wale waliomzunguka walipoona jambo lililokuwa karibu kutukia, wakasema: “Bwana, tuwashambulie kwa upanga?” 50 Mmoja wao hata akampiga mtumwa wa kuhani mkuu na kumkata sikio la kulia.+ 51 Lakini Yesu akasema: “Inatosha.” Akaligusa sikio la yule mtumwa akamponya. 52 Kisha Yesu akawauliza wakuu wa makuhani na makapteni wa hekalu na wazee waliokuja kumkamata: “Je, mmekuja kunikamata mkiwa na mapanga na marungu kana kwamba mimi ni mwizi?+ 53 Nilipokuwa pamoja nanyi hekaluni siku baada ya siku,+ hamkunikamata.+ Lakini huu ndio wakati wenu na mamlaka ya giza.”+
54 Ndipo wakamkamata,+ na kumpeleka nyumbani kwa kuhani mkuu; lakini Petro alikuwa akiwafuata kwa mbali.+ 55 Walipowasha moto katikati ya ua na kuketi chini pamoja, Petro alikuwa ameketi miongoni mwao.+ 56 Lakini kijakazi mmoja akamwona Petro akiwa ameketi kando ya moto, akamtazama kwa makini na kusema: “Mtu huyu pia alikuwa pamoja naye.” 57 Lakini Petro akakana, akisema: “Wewe mwanamke, mimi simjui.” 58 Baadaye kidogo mtu mwingine akamwona na kusema: “Wewe pia ni mmoja wao.” Lakini Petro akasema: “Mimi si mmoja wao.”+ 59 Baada ya saa moja hivi kupita mwanamume mwingine akaanza kusisitiza kwa nguvu: “Kwa hakika mtu huyu pia alikuwa pamoja naye, kwa maana, yeye ni Mgalilaya!” 60 Lakini Petro akasema: “Wewe mtu, mimi sielewi unachosema.” Mara tu alipokuwa akisema, jogoo akawika. 61 Ndipo Bwana akageuka, akamtazama Petro moja kwa moja, naye Petro akakumbuka maneno ambayo Bwana alimwambia: “Kabla jogoo hajawika leo, utanikana mara tatu.”+ 62 Naye akaenda nje akalia kwa uchungu.
63 Sasa wale wanaume waliokuwa wamemkamata Yesu wakaanza kumdhihaki+ na kumpiga;+ 64 na baada ya kumfunika uso wakawa wakisema: “Toa unabii! Ni nani aliyekupiga?” 65 Nao wakasema mambo mengine mengi ya kumkufuru.
66 Kulipokuwa mchana, kikundi cha wazee wa watu, yaani, wakuu wa makuhani na waandishi, wakakusanyika pamoja,+ nao wakampeleka katika jumba lao la Sanhedrini, na kumwambia: 67 “Ikiwa wewe ndiye Kristo, tuambie.”+ Lakini akasema: “Hata nikiwaambia, hamtaamini hata kidogo. 68 Isitoshe, ikiwa ningewauliza, hamngenijibu. 69 Hata hivyo, tangu sasa Mwana wa binadamu+ ataketi kwenye mkono wa kuume wenye nguvu wa Mungu.”+ 70 Ndipo wote wakasema: “Kwa hiyo, je, wewe ndiye Mwana wa Mungu?” Akawajibu: “Ninyi wenyewe mnasema kwamba mimi ndiye.” 71 Wakasema: “Kwa nini tutafute ushahidi zaidi? Kwa maana sisi wenyewe tumesikia kutoka kinywani mwake.”+
23 Kisha umati huo wote ukasimama na kumpeleka Yesu kwa Pilato.+ 2 Ndipo wakaanza kumshtaki,+ wakisema: “Tulimkuta mtu huyu akipindua taifa letu na kuwakataza watu wasimlipe Kaisari kodi,+ akisema kwamba yeye mwenyewe ni Kristo mfalme.”+ 3 Sasa Pilato akamuuliza: “Je, wewe ndiye Mfalme wa Wayahudi?” Akamjibu: “Wewe mwenyewe unasema hivyo.”+ 4 Ndipo Pilato akawaambia wakuu wa makuhani na ule umati: “Sioni mtu huyu akiwa na kosa lolote.”+ 5 Lakini wakasisitiza wakisema: “Anawachochea watu kwa kufundisha katika Yudea yote, kuanzia Galilaya mpaka hapa.” 6 Pilato aliposikia hivyo akauliza ikiwa Yesu alikuwa Mgalilaya. 7 Baada ya kuhakikisha kwamba alitoka katika eneo lililotawaliwa na Herode, akaagiza apelekwe kwa Herode,+ ambaye pia siku hizo alikuwa Yerusalemu.
8 Herode alipomwona Yesu alifurahi sana. Kwa maana kwa muda mrefu alitaka kumwona Yesu kwa sababu alikuwa amesikia mengi kumhusu,+ na alitamani kumwona akifanya miujiza. 9 Basi akaanza kumuuliza maswali mengi, lakini Yesu hakumjibu.+ 10 Hata hivyo, wakuu wa makuhani na waandishi wakaendelea kusimama na kumshtaki kwa ukali. 11 Ndipo Herode na wanajeshi wake wakamtendea kwa dharau,+ naye Herode akamdhihaki+ kwa kumvika vazi la kifahari na kuagiza arudishwe kwa Pilato. 12 Siku hiyo Herode na Pilato wakawa marafiki, kwa maana kabla ya hapo walikuwa maadui.
13 Ndipo Pilato akawaita wakuu wa makuhani, watawala, na watu, 14 akawaambia: “Mliniletea mtu huyu mkisema anachochea watu kuasi. Tazama! Nilimhoji mbele yenu lakini sikupata msingi wa mashtaka yenu dhidi yake.+ 15 Kwa kweli, hata Herode hakupata, ndiyo maana alimrudisha kwetu, tazama! ni wazi hajafanya jambo lolote linalostahili kifo. 16 Kwa hiyo nitamwadhibu+ na kumfungua.” 17* —— 18 Lakini umati wote ukasema kwa sauti kubwa: “Muue mtu huyu,* na utufungulie Baraba!”+ 19 (Mtu huyo alikuwa amefungwa gerezani kwa sababu ya mauaji na uchochezi uliokuwa umetokea jijini.) 20 Pilato akawapazia sauti tena, kwa sababu alitaka kumfungua Yesu.+ 21 Ndipo wakaanza kupiga kelele, wakisema: “Atundikwe mtini! Atundikwe mtini!”*+ 22 Akawaambia mara ya tatu: “Kwa nini? Amefanya kosa gani? Mimi sikuona jambo lolote linalofanya astahili kifo; kwa hiyo nitamwadhibu kisha nimfungue.” 23 Lakini wakazidi kusisitiza, wakidai kwa sauti kubwa, kwamba auawe,* na sauti zao zikashinda.+ 24 Basi Pilato akaamua kutimiza dai lao. 25 Akamfungua yule mtu waliyemtaka, ambaye alikuwa amefungwa gerezani kwa sababu ya uchochezi na mauaji, lakini akamkabidhi Yesu mikononi mwao ili wamtendee wanavyopenda.
26 Walipokuwa wakienda naye, wakamshika Simoni wa Kirene, aliyekuwa akitoka mashambani, nao wakamtwika mti wa mateso* aubebe na kumfuata Yesu.+ 27 Watu wengi walikuwa wakimfuata, kutia ndani wanawake waliokuwa wakijipigapiga kwa huzuni na kumwombolezea. 28 Yesu akawageukia wanawake hao na kuwaambia: “Binti za Yerusalemu, acheni kunililia. Bali jililieni ninyi wenyewe na watoto wenu;+ 29 kwa maana tazama! siku zinakuja ambapo watu watasema, ‘Wenye furaha ni wanawake walio tasa, wanawake ambao hawakuzaa, na wanawake ambao hawakunyonyesha!’+ 30 Ndipo wataanza kuiambia milima, ‘Tuangukieni!’ na vilima, ‘Tufunikeni!’+ 31 Ikiwa wanafanya mambo haya wakati mti ni mbichi, itakuwaje utakapokauka?”
32 Wanaume wengine wawili, wahalifu, walikuwa pia wakipelekwa wakauawe pamoja naye.+ 33 Walipofika mahali panapoitwa Fuvu la Kichwa,+ wakamtundika Yesu kwenye mti pamoja na wale wahalifu, mmoja upande wake wa kuume na mwingine upande wake wa kushoto.+ 34 Lakini Yesu alikuwa akisema: “Baba, wasamehe, kwa maana hawajui wanachofanya.” Isitoshe, wakapiga kura ili wagawane mavazi yake.+ 35 Watu walikuwa wamesimama hapo wakitazama. Lakini wale viongozi walikuwa wakimdhihaki na kusema: “Aliwaokoa wengine; mwacheni ajiokoe mwenyewe, ikiwa yeye ndiye Yule Aliyechaguliwa, Kristo wa Mungu.”+ 36 Hata wale wanajeshi wakamdhihaki, wakamkaribia na kumpa divai kali+ 37 wakisema: “Ikiwa wewe ndiye Mfalme wa Wayahudi, jiokoe.” 38 Kulikuwa pia na maandishi haya juu yake: “Huyu ndiye Mfalme wa Wayahudi.”+
39 Ndipo mmoja wa wale wahalifu waliotundikwa akaanza kumtukana+ akisema: “Wewe ndiye Kristo, sivyo? Jiokoe na utuokoe sisi pia!” 40 Yule mwingine akamkemea akisema: “Je, wewe humwogopi Mungu hata kidogo, kwa kuwa umepata hukumu ileile? 41 Sisi tunastahili kuteseka kwa sababu ya makosa tuliyofanya; lakini mtu huyu hakufanya kosa lolote.” 42 Kisha akasema: “Yesu, unikumbuke utakapoingia katika Ufalme wako.”+ 43 Yesu akamwambia: “Kwa kweli ninakuambia leo, utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”+
44 Sasa, karibu saa sita,* kukawa na giza katika nchi yote mpaka saa tisa,*+ 45 kwa sababu hakukuwa na nuru ya jua; kisha pazia la patakatifu+ likapasuka katikati.+ 46 Naye Yesu akapaza sauti na kusema: “Baba, naiweka roho yangu mikononi mwako.”+ Baada ya kusema hayo akafa.*+ 47 Alipoona mambo yaliyotokea, ofisa wa jeshi akaanza kumtukuza Mungu, akisema: “Kwa kweli mtu huyu alikuwa mwadilifu.”+ 48 Na watu wote waliokuwa wamekusanyika hapo ili kuona tukio hilo, walipoona mambo yaliyotukia, wakarudi nyumbani wakijipigapiga vifua. 49 Wale wote waliomfahamu walikuwa wamesimama mbali kidogo. Pia, wanawake waliokuwa wamefuatana naye kutoka Galilaya, walikuwa hapo na waliona mambo hayo.+
50 Na tazama! kulikuwa na mwanamume aliyeitwa Yosefu, mshiriki wa Baraza, ambaye alikuwa mtu mwema na mwadilifu.+ 51 (Mtu huyo hakupiga kura kuunga mkono njama na kitendo chao.) Alikuwa wa kutoka Arimathea, jiji la Wayudea, naye alikuwa akiungojea Ufalme wa Mungu. 52 Mtu huyo alienda kwa Pilato akaomba apewe mwili wa Yesu. 53 Naye akaushusha+ na kuufunga kwa kitani bora, akaulaza katika kaburi* lililochongwa kwenye mwamba,+ ambamo hakuna mtu aliyewahi kulazwa. 54 Ilikuwa siku ya Matayarisho,+ na Sabato+ ilikuwa inakaribia kuanza. 55 Lakini wanawake waliokuja naye kutoka Galilaya, wakaenda kutazama kaburi* na jinsi mwili wake ulivyolazwa,+ 56 kisha wakarudi kutayarisha manukato na mafuta yenye marashi. Lakini, bila shaka, walipumzika siku ya Sabato+ kulingana na Sheria.
24 Hata hivyo, siku ya kwanza ya juma asubuhi na mapema, walienda kwenye kaburi,* wakiwa na manukato waliyotayarisha.+ 2 Lakini wakakuta jiwe limeviringishwa kutoka kwenye kaburi,*+ 3 nao walipoingia, hawakuupata mwili wa Bwana Yesu.+ 4 Wakiwa wameshangazwa na jambo hilo, tazama! wanaume wawili waliovaa mavazi yanayong’aa wakasimama kando yao. 5 Wanawake hao wakaogopa sana wakainamisha nyuso zao, basi wale wanaume wakawaambia: “Kwa nini mnamtafuta yule aliye hai kati ya wafu?+ 6 Hayupo hapa, amefufuliwa. Kumbukeni jinsi alivyowaambia alipokuwa Galilaya, 7 kwamba Mwana wa binadamu lazima atiwe mikononi mwa wenye dhambi na kuuawa kwenye mti na siku ya tatu afufuliwe.”+ 8 Ndipo wakakumbuka maneno yake,+ 9 wakarudi kutoka kaburini,* wakawaambia mambo hayo yote wale 11 na wengine wote.+ 10 Walikuwa Maria Magdalene, Yoana, na Maria mama ya Yakobo. Pia, wanawake wengine waliokuwa pamoja nao waliwaambia mitume mambo hayo. 11 Hata hivyo, waliyaona maneno hayo kama upuuzi, nao hawakuwaamini wanawake hao.
12 Lakini Petro akatoka, akakimbia hadi kwenye kaburi,* na alipoinama mbele, akaona vile vitambaa vya kitani peke yake. Kwa hiyo akaondoka akiwa ameshangazwa na mambo yaliyotokea.
13 Lakini tazama! siku hiyohiyo wanafunzi wawili walikuwa wakisafiri kwenda kijiji kinachoitwa Emau, kilicho karibu kilomita 11* kutoka Yerusalemu, 14 nao walikuwa wakizungumza kuhusu mambo hayo yote yaliyotukia.
15 Sasa walipokuwa wakiongea na kujadiliana kuhusu mambo hayo, Yesu akakaribia na kuanza kutembea pamoja nao, 16 lakini macho yao yalizuiwa wasiweze kumtambua.+ 17 Akawauliza: “Ni mambo gani haya mnayojadiliana huku mkitembea?” Nao wakasimama tuli, wakiwa na huzuni. 18 Yule aliyeitwa Kleopa akamjibu: “Je, wewe ni mgeni anayekaa peke yake Yerusalemu hivi kwamba hujui* mambo ambayo yametukia huko siku hizi?” 19 Akawauliza: “Mambo gani?” Wakamjibu: “Kuhusu Yesu Mnazareti,+ yule nabii aliyefanya miujiza na kusema maneno yenye nguvu mbele za Mungu na watu wote;+ 20 na jinsi wakuu wa makuhani wetu na watawala walivyomtoa ili ahukumiwe kifo,+ kisha wakamtundika kwenye mti. 21 Tulitazamia kwamba yeye ndiye angekomboa Israeli.+ Ndiyo, isitoshe hii ni siku ya tatu tangu mambo hayo yatokee. 22 Pia, wanawake fulani miongoni mwetu walitushangaza, kwa sababu walienda mapema kwenye kaburi*+ 23 na walipokosa kuuona mwili wake, wakarudi wakisema pia waliona maono yasiyo ya kawaida ya malaika waliowaambia kwamba Yesu yuko hai. 24 Kisha baadhi ya wenzetu wakaenda kwenye kaburi,*+ wakalikuta kama vile wale wanawake walivyosema, lakini hawakumwona.”
25 Basi akawaambia: “Enyi wasio na akili na wagumu kuamini mambo yote yaliyosemwa na manabii! 26 Je, haikuwa lazima Kristo kupatwa na mateso haya+ kisha aingie kwenye utukufu wake?”+ 27 Naye akawafafanulia kuanzia Musa na Manabii wote,+ mambo yote ambayo Maandiko yalisema kumhusu.
28 Mwishowe walipokaribia kijiji walichokuwa wakienda, Yesu akajifanya kana kwamba anaendelea na safari. 29 Lakini wakamsihi asiende, wakisema: “Kaa pamoja nasi, kwa sababu ni jioni, na siku inakaribia kwisha.” Basi akaingia ili akae pamoja nao. 30 Naye alipokuwa akila* pamoja nao akauchukua mkate, akaubariki, akaumega na kuanza kuwapa.+ 31 Ndipo macho yao yakafunguliwa kikamili nao wakamtambua; lakini akatoweka.+ 32 Wakaambiana: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akizungumza nasi barabarani, na alipokuwa akitufungulia* Maandiko waziwazi?” 33 Saa hiyohiyo wakaondoka na kurudi Yerusalemu, wakawakuta wale 11 na watu waliokusanyika pamoja nao, 34 wakasema: “Kwa kweli Bwana alifufuliwa naye alimtokea Simoni!”+ 35 Kisha wakasimulia mambo yaliyotokea barabarani na jinsi walivyomtambua alipoumega mkate.+
36 Walipokuwa wakisema mambo hayo Yesu akasimama katikati yao na kuwaambia: “Na muwe na amani.”+ 37 Lakini kwa sababu walikuwa wameshtuka na kuogopa, walidhani kwamba wanaona roho. 38 Basi akawauliza: “Kwa nini mnahangaika, na kwa nini mna shaka mioyoni mwenu? 39 Angalieni mikono na miguu yangu, kwamba ni mimi; niguseni mwone, kwa maana roho haina nyama na mifupa kama vile mnavyoona nilivyo.” 40 Alipokuwa akisema hayo, akawaonyesha mikono yake na miguu yake. 41 Wakiwa bado hawaamini kwa sababu ya shangwe nyingi na mshangao, akawauliza: “Mna chakula chochote hapa?” 42 Basi wakampa kipande cha samaki wa kuchomwa, 43 akakichukua, akala wakimtazama.
44 Kisha akawaambia: “Haya ndiyo maneno niliyowaambia nilipokuwa bado pamoja nanyi,+ kwamba mambo yote yaliyoandikwa kunihusu katika Sheria ya Musa, Manabii, na Zaburi lazima yatimizwe.”+ 45 Ndipo akafungua akili zao ili waelewe kabisa maana ya Maandiko,+ 46 naye akawaambia: “Imeandikwa kwamba Kristo atateseka na kufufuliwa kutoka kwa wafu siku ya tatu,+ 47 na kwa msingi wa jina lake, toba kwa msamaha wa dhambi+ ingehubiriwa katika mataifa yote+—kuanzia Yerusalemu.+ 48 Ninyi mtakuwa mashahidi wa mambo haya.+ 49 Na tazama! Nitawatumia kile ambacho Baba yangu ameahidi. Hata hivyo, kaeni jijini mpaka mtakapovikwa nguvu kutoka juu.”+
50 Kisha akawaongoza mpaka Bethania, naye akainua mikono yake na kuwabariki. 51 Alipokuwa akiwabariki akatenganishwa nao, akaanza kuchukuliwa juu mbinguni.+ 52 Wakamsujudia* na kurudi Yerusalemu wakiwa na shangwe kubwa.+ 53 Nao walikuwa hekaluni kila siku wakimsifu Mungu.+
Angalia Kamusi.
Angalia Nyongeza A5.
Au “zoea la.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Au “tangu akiwa katika tumbo la mama yake.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Au “maono.”
Au “utumishi wake wa watu wote.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Au “utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “jambo lolote.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Kamusi.
Angalia Nyongeza A5.
Tnn., “mbegu yake.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Au “mwokozi mwenye nguvu.” Angalia Kamusi, “Pembe.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Au “watu wenye kibali chake.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Tnn., “anayefungua tumbo la uzazi.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Au “utaji.”
Au “utakuchoma nafsi yako.”
Tnn., “tangu alipokuwa bikira.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “akabaki mtiifu.”
Yaani, Herode Antipa. Angalia Kamusi.
Tnn., “tetraki.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “wanadamu wote.”
Au “njia ya Mungu ya kuokoa.”
Au “nyoka-vipiri.”
Au “vazi la ziada.”
Au “Msikusanye.”
Au “Msimdhulumu.”
Au “mishahara yenu.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “ukuta wa ukingoni wa; sehemu ya juu zaidi ya.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Au “aliyeponywa.”
Au “kumwinda”
Yaani, Bahari ya Galilaya.
Tnn., “wakazingira.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “machela.”
Au “walikuwa wameketi mezani.”
Au “mikate ya wonyesho.”
Au “nafsi.”
Au “kukataa jina lenu.”
Yaani, mkiwakopesha bila faida.
Au “kuachilia.”
Au “mtaachiliwa.”
Tnn., “mwana mzaliwa pekee.”
Au “machela ya kubebea maiti.”
Au “mavazi bora?”
Tnn., “mbele ya uso wako.”
Au “mwongozo wa.”
Au “hutetewa.”
Au “kupitia matokeo yake.”
Au “alikuwa ameketi mezani.”
Angalia Nyongeza B14.
Au “kubwa.”
Au “makaburi ya ukumbusho.”
Au labda, “alikuwa amemshika kwa muda mrefu.”
Au “abiso.” Angalia Kamusi.
Au “ukingo wenye mteremko mkali.”
Tnn., “mzaliwa pekee.”
Au “nguvu za uhai zikarudi.”
Tnn., “fedha.”
Au “vazi la ziada.”
Yaani, Herode Antipa. Angalia Kamusi.
Tnn., “tetraki.”
Angalia Kamusi.
Au “nafsi yake.”
Au “nafsi yake.”
Tnn., “ulipotimia.”
Tnn., “alikuwa ameelekeza uso wake.”
Au “kumsalimu kwa kumkumbatia”
Au “Hadesi.” Angalia Kamusi.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Kamusi.
Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “neno lake.”
Au “fungu bora.”
Au “litukuzwe; lionwe kuwa takatifu.”
Jina lingine la Shetani.
Au “kikapu cha kupimia.”
Au “linaona vizuri.” Tnn., “ni rahisi.”
Au “utajawa na nuru.”
Tnn., “ni baya; lina uovu.”
Yaani, hakujisafisha kisherehe.
Au “ili kuwapa maskini zawadi.” Angalia Kamusi.
Au “vilivyo bora.”
Au “makaburi ya ukumbusho.”
Au “makaburi yasiyo na alama.”
Au “makaburi ya ukumbusho.”
Au “hekalu.”
Au “kitashtakiwa.”
Angalia Kamusi.
Tnn., “kwa sarafu mbili za asarioni. ” Angalia Nyongeza B14.
Au “hampuuzi.”
Au “masinagogi.”
Au “tamaa.”
Au “nitaiambia nafsi yangu.”
Au “Nafsi, una”
Au “nafsi yako.”
Au “nafsi zenu.”
Au “nafsi ina.”
Angalia Nyongeza B14.
Aina ya maua.
Au “kuwapa maskini zawadi.” Angalia Kamusi.
Aina ya wadudu.
Tnn., “Jifungeni mishipi viunoni.”
Au “atajifunga kiunoni.”
Kuanzia saa 3 usiku mpaka saa 6 usiku.
Kuanzia saa 6 usiku mpaka saa 9 usiku.
Au “msimamizi wa nyumba.”
Au “mwenye hekima.”
Au “watumishi wa nyumbani.”
Au “kufanya mapenzi yake.”
Tnn., “leptoni ya mwisho.” Angalia Nyongeza B14.
Au “roho mwovu aliyemlemaza.”
Au “hamira.”
Tnn., “vipimo vya sea.” Sea moja ilikuwa sawa na kilogramu 3.3 au lita 7.33. Angalia Nyongeza B14.
Au “ukaumuka.”
Au “ni jambo lisilowaziwa.”
Angalia Nyongeza A5.
Uvimbe unaosababishwa na umajimaji kuongezeka mwilini.
Tnn., “anayekula mkate.”
Au “ng’ombe kumi.”
Au “hampendi kwa kiwango kidogo zaidi.”
Au “nafsi yake.”
Angalia Kamusi, “Mti wa mateso.”
Au “asipoacha.”
Angalia Nyongeza B14.
Angalia Nyongeza B14.
Au “wanawake ambao ni rafiki zake.”
Angalia Nyongeza B14.
Au “upotovu; bila kujali.”
Tnn., “akamwangukia shingoni.”
Au “amerudi salama.”
Tnn., “aliyekula; aliyeharibu.”
Au “msimamizi wa nyumba.”
Au “vipimo vya bathi.” Bathi moja ilikuwa sawa na lita 22. Angalia Nyongeza B14.
Au “vipimo 100 vya kori.” Kori moja ilikuwa sawa na kilogramu 170. Angalia Nyongeza B14.
Au “kwa busara; kwa werevu.”
Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Tnn., “kwenye kifua cha Abrahamu.”
Au “Hadesi.” Angalia Kamusi.
Tnn., “kwenye kifua chake.”
Au “tuonyeshe rehema!”
Au “uko miongoni mwenu.”
Au “nafsi yake.”
Angalia Nyongeza A3.
Au “kunishambulia mpaka animalize.”
Au “imani kama hii.” Tnn., “ile imani.”
Au “nionyeshe rehema.”
Angalia Kamusi.
Au “yatakamilika.”
Au “nionyeshe rehema!”
Au “nionyeshe rehema!”
Au “mforsadi-tini.”
Au “nilichomnyang’anya kwa shtaka la uwongo.”
Mina ya Ugiriki ilikuwa na uzito wa gramu 340 na ilikuwa na thamani ya drakma 100. Angalia Nyongeza B14.
Au “ufalme.”
Tnn., “fedha.”
Tnn., “fedha.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “watakutaabisha.”
Au “chanzo chake ni wanadamu?”
Au “wakamvunjia heshima.”
Tnn., “kichwa cha pembeni.”
Au “sawa.”
Au “kodi ya kichwa.”
Angalia Nyongeza B14.
Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “kwa maoni yake.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “vilivyo bora.”
Au “mali.”
Au “kuwa kisingizio.”
Au “nzito.”
Au “makasha.”
Tnn., “leptoni mbili.” Angalia Nyongeza B14.
Au, “mwenye uhitaji.”
Au “misukosuko.”
Au “mtasalitiwa.”
Au “mtapata nafsi zenu.”
Au “siku za kisasi.”
Au “Watu wa mataifa.”
Au “Watu wa mataifa.”
Au “anayeketi mezani.”
Au “mtumishi.”
Au “anayeketi mezani.”
Au “mtumishi.”
Angalia Nyongeza A3.
Tnn., “Mwondoe mtu huyu.”
Au “Auawe kwenye mti! Auawe kwenye mti!”
Au “auawe kwenye mti.”
Angalia Kamusi.
Yaani, karibu saa 6 mchana.
Yaani, karibu saa 9 alasiri.
Au “akakata pumzi.”
Au “kaburi la ukumbusho.”
Au “kaburi la ukumbusho.”
Au “kaburi la ukumbusho.”
Au “kaburi la ukumbusho.”
Au “kwenye kaburi la ukumbusho.”
Au “kaburi la ukumbusho.”
Tnn., “stadia 60.” Stadia moja ilikuwa sawa na mita 185 (futi 606.95). Angalia Nyongeza B14.
Au labda, “Je, wewe ni mgeni pekee katika Yerusalemu ambaye hajui?”
Au “kaburi la ukumbusho.”
Au “kaburi la ukumbusho.”
Au “alipokuwa ameketi mezani.”
Au “akitufafanulia.”
Au “Wakamwinamia.”