Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt Kumbukumbu la Torati 1:1-34:12
  • Kumbukumbu la Torati

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumbukumbu la Torati
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Kumbukumbu la Torati

KUMBUKUMBU LA TORATI

1 Haya ndiyo maneno ambayo Musa aliwaambia Waisraeli wote walipokuwa nyikani katika eneo la Yordani, katika jangwa tambarare mbele ya Sufi, kati ya Parani, Tofeli, Labani, Haserothi, na Dizahabu. 2 Ni safari ya siku 11 kutoka Horebu mpaka Kadesh-barnea+ kupitia njia ya Mlima Seiri. 3 Katika mwaka wa 40,+ mwezi wa 11, siku ya kwanza ya mwezi huo, Musa aliwaambia Waisraeli* mambo yote ambayo Yehova alimwagiza awaambie. 4 Alifanya hivyo baada ya kumshinda Sihoni+ mfalme wa Waamori, aliyekuwa akikaa Heshboni, na Ogu+ mfalme wa Bashani, aliyekuwa akikaa Ashtarothi, kule Edrei.+ 5 Katika eneo la Yordani nchini Moabu, Musa alianza kuifafanua Sheria+ akisema:

6 “Yehova Mungu wetu alituambia hivi kule Horebu: ‘Mmekaa muda wa kutosha katika eneo hili lenye milima.+ 7 Geukeni na kuelekea katika eneo lenye milima la Waamori+ na kwa majirani wao wote kule Araba,+ katika eneo lenye milima, Shefela, Negebu, pwani ya bahari,+ nchi ya Wakanaani, na Lebanoni,*+ hadi kwenye ule mto mkubwa, Mto Efrati.+ 8 Angalieni, nimeweka nchi hii mbele yenu. Ingieni mwimiliki nchi ambayo mimi Yehova niliapa kwamba nitawapa baba zenu, Abrahamu, Isaka,+ na Yakobo,+ wao pamoja na uzao wao* baada yao.’+

9 “Nami niliwaambia ninyi wakati huo, ‘Siwezi kuwabeba peke yangu.+ 10 Yehova Mungu wenu amewafanya mwongezeke, nanyi leo ni wengi kama nyota za mbinguni.+ 11 Yehova Mungu wa mababu zenu na awafanye mwongezeke+ mara elfu moja zaidi ya mlivyo sasa, na awabariki kama alivyowaahidi.+ 12 Mimi peke yangu ninawezaje kuwabeba ninyi ambao ni mzigo pamoja na mizigo yenu na ugomvi wenu?+ 13 Chagueni wanaume wenye hekima, busara, na wenye uzoefu kutoka katika makabila yenu, nami nitawaweka kuwa viongozi wenu.’+ 14 Mkanijibu, ‘Jambo ulilotuambia ni jema.’ 15 Basi nikawachukua viongozi wa makabila yenu, wanaume wenye hekima na uzoefu, na kuwaweka kuwa viongozi wenu, wakuu wa maelfu, wakuu wa mamia, wakuu wa hamsini, wakuu wa makumi, na maofisa wa makabila yenu.+

16 “Wakati huo niliwaagiza hivi waamuzi wenu: ‘Mnaposikiliza kesi kati ya ndugu zenu, mnapaswa kuhukumu kwa uadilifu+ kati ya mtu na ndugu yake au mkaaji mgeni.+ 17 Hampaswi kuhukumu kwa upendeleo.+ Mnapaswa kumsikiliza mdogo kama mnavyomsikiliza mkubwa.+ Msiogopeshwe na wanadamu,+ kwa sababu hukumu ni ya Mungu;+ na ikiwa kesi ni ngumu sana kwenu, ileteni kwangu, nami nitaisikiliza.’+ 18 Wakati huo niliwapa maagizo kuhusu mambo yote mnayopaswa kufanya.

19 “Kisha tukaondoka Horebu na kupitia ile nyika yote kubwa na yenye kutisha+ mliyoona njiani kuelekea kwenye eneo lenye milima la Waamori,+ kama Yehova Mungu wetu alivyotuamuru, na mwishowe tukafika Kadesh-barnea.+ 20 Halafu nikawaambia, ‘Mmefika kwenye eneo lenye milima la Waamori, ambalo Yehova Mungu wetu anatupatia. 21 Angalieni, Yehova Mungu wenu amewapa nchi hii. Pandeni, mkaimiliki, kama Yehova, Mungu wa mababu zenu alivyowaambia.+ Msiogope wala msiwe na hofu.’

22 “Hata hivyo, ninyi nyote mlinijia na kusema, ‘Na tutume wanaume watutangulie na kuipeleleza nchi kwa ajili yetu, watuletee habari kuhusu njia tunayopaswa kufuata na ni majiji ya aina gani tutakayoyapata huko.’+ 23 Pendekezo hilo lilionekana zuri kwangu, kwa hiyo nikawachagua wanaume 12 miongoni mwa wanaume wenu, mwanamume mmoja kwa ajili ya kila kabila.+ 24 Wakaondoka na kupanda kwenda kwenye eneo lenye milima,+ wakafika kwenye Bonde la Eshkoli na kuipeleleza nchi. 25 Wakachukua baadhi ya matunda ya nchi hiyo na kutuletea, nao wakatuletea habari hii: ‘Nchi ambayo Yehova Mungu wetu anatupatia ni nzuri.’+ 26 Lakini mlikataa kupanda kwenda huko, nanyi mkaliasi agizo la Yehova Mungu wenu.+ 27 Mliendelea kunung’unika katika mahema yenu na kusema, ‘Yehova alituchukia ndiyo sababu alitutoa katika nchi ya Misri ili atutie mikononi mwa Waamori watuangamize. 28 Tunaenda mahali pa aina gani? Ndugu zetu walituvunja moyo*+ waliposema, “Watu hao wana nguvu zaidi na ni warefu zaidi kuliko sisi, na majiji yao ni makubwa na yana ngome zinazofika mbinguni,*+ na huko tuliwaona wana wa Waanaki.”’+

29 “Kwa hiyo nikawaambia, ‘Msiwe na hofu wala msiogope kwa sababu yao.+ 30 Yehova Mungu wenu atawatangulia na kuwapigania,+ kama alivyofanya kule Misri mbele ya macho yenu wenyewe.+ 31 Nanyi mliona nyikani jinsi Yehova Mungu wenu alivyowabeba kama baba anavyombeba mwana wake, aliwabeba kila mahali mlipoenda mpaka mlipofika mahali hapa.’ 32 Lakini licha ya hayo yote, hamkuwa na imani katika Yehova Mungu wenu,+ 33 aliyekuwa akiwatangulia njiani ili apeleleze mahali mtakapopiga kambi. Alitokea kwa moto wakati wa usiku na kwa wingu wakati wa mchana ili awaonyeshe njia mnayopaswa kufuata.+

34 “Wakati huo wote Yehova alisikia mambo mliyokuwa mkisema, akakasirika na kuapa hivi:+ 35 ‘Hakuna mtu hata mmoja wa kizazi hiki kiovu atakayeona nchi nzuri niliyoapa kwamba nitawapa baba zenu,+ 36 isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune. Yeye ataiona, nami nitampa yeye na wanawe nchi hiyo aliyoikanyaga kwa miguu yake, kwa sababu amenifuata mimi Yehova kwa moyo wote.*+ 37 (Yehova alinikasirikia mimi pia kwa sababu yenu, akasema, “Wewe pia hutaingia humo.+ 38 Yoshua mwana wa Nuni, mtumishi wako,*+ ndiye atakayeingia katika nchi hiyo.+ Mwimarishe,*+ kwa maana atawawezesha Waisraeli kuirithi nchi hiyo.”) 39 Isitoshe, watoto wenu ambao mlisema watakuwa nyara+ na wana wenu ambao leo hawajui lililo jema wala baya, hao ndio watakaoingia katika nchi hiyo, nami nitawapa ili waimiliki.+ 40 Lakini ninyi, geukeni na kwenda nyikani kupitia njia ya Bahari Nyekundu.’+

41 “Ndipo mliponiambia, ‘Tumemtendea Yehova dhambi. Sasa tutapanda kwenda kupigana, kama Yehova Mungu wetu alivyotuamuru!’ Basi kila mmoja wenu akajivika silaha zake za vita, nanyi mlifikiri ni rahisi kupanda mlimani.+ 42 Lakini Yehova akaniambia, ‘Waambie, “Msipande kwenda kupigana, kwa sababu sitakuwa pamoja nanyi.+ Mkienda, maadui wenu watawashinda.”’ 43 Basi nikaongea nanyi, lakini hamkusikiliza. Badala yake, mliasi agizo la Yehova na kujaribu kwa kimbelembele kupanda mlimani. 44 Kisha Waamori waliokuwa wakikaa kwenye mlima huo wakatoka ili kuwashambulia, wakawakimbiza kama nyuki wanavyofanya na kuwatawanya kuanzia Seiri mpaka Horma. 45 Basi mkarudi na kuanza kumlilia Yehova, lakini Yehova hakuwasikiliza wala kuwakazia uangalifu. 46 Ndiyo sababu mliendelea kukaa Kadeshi kwa muda wote mliokaa huko.

2 “Kisha tukageuka na kwenda nyikani kupitia njia ya Bahari Nyekundu, kama Yehova alivyoniambia,+ nasi tulizunguka-zunguka Mlima Seiri kwa siku nyingi. 2 Mwishowe Yehova akaniambia hivi: 3 ‘Mmeuzunguka-zunguka mlima huu kwa muda mrefu vya kutosha. Sasa geukeni mwelekee kaskazini. 4 Nawe uwaamuru watu hivi: “Mtapita karibu na mpaka wa ndugu zenu, wazao wa Esau,+ wanaokaa Seiri,+ nao watawaogopa ninyi,+ basi mnapaswa kuwa waangalifu sana. 5 Msizozane nao,* kwa sababu sitawapa sehemu yoyote ya nchi yao, hata mahali panapotoshea wayo wa mguu, kwa sababu nimempa Esau Mlima Seiri uwe miliki yake.+ 6 Mnapaswa kuwalipa pesa kwa ajili ya chakula mtakachokula, nanyi mnapaswa kulipia maji mtakayokunywa.+ 7 Kwa maana Yehova Mungu wenu amewabariki katika mambo yote mliyofanya. Anajua vizuri kabisa safari yenu katika nyika hii kubwa. Yehova Mungu wenu amekuwa pamoja nanyi kwa miaka hii 40, nanyi hamjakosa kitu chochote.”’+ 8 Basi tuliwapita ndugu zetu, wazao wa Esau,+ wanaokaa Seiri, tukaepuka njia ya Araba, kutoka Elathi na kutoka Esion-geberi.+

“Kisha tukageuka na kupitia njia ya nyika ya Moabu.+ 9 Ndipo Yehova akaniambia, ‘Msizozane wala kupigana na Wamoabu, kwa sababu sitawapa ninyi sehemu yoyote ya nchi yao ili mwimiliki kwa sababu nimewapa wazao wa Loti+ nchi ya Ari ili waimiliki. 10 (Waemi+ waliishi katika nchi hiyo zamani, walikuwa watu wenye nguvu na wengi sana na warefu kama Waanaki. 11 Warefaimu+ pia walionwa kama Waanaki,+ na Wamoabu walikuwa wakiwaita Waemi. 12 Awali, Wahori+ waliishi Seiri, lakini wazao wa Esau walimiliki nchi yao, wakawaangamiza na kukaa humo badala yao,+ kama Waisraeli watakavyofanya katika nchi ambayo ni miliki yao, ambayo kwa hakika Yehova atawapa.) 13 Sasa nendeni mvuke Bonde* la Zeredi.’ Basi tukavuka Bonde la Zeredi.+ 14 Tulitembea kwa miaka 38 kutoka Kadesh-barnea mpaka tulipovuka Bonde la Zeredi, mpaka kizazi chote cha wanaume wa vita kilipoangamia kutoka kambini, kama Yehova alivyokuwa amewaapia.+ 15 Mkono wa Yehova uliwapinga ili kuwaangamiza kutoka kambini mpaka walipoisha.+

16 “Mara tu wanaume wote wa vita walipokufa,+ 17 Yehova akazungumza nami tena, akaniambia, 18 ‘Leo mtapita karibu na eneo la Moabu, yaani, Ari. 19 Mtakapofika karibu na Waamoni, msiwachokoze wala kuzozana nao, kwa sababu sitawapa ninyi nchi yoyote ya Waamoni ili mwimiliki, kwa kuwa nimewapa wazao wa Loti waimiliki.+ 20 Nchi hiyo pia ilionwa kuwa nchi ya Warefaimu.+ (Warefaimu waliishi katika nchi hiyo zamani, na Waamoni walikuwa wakiwaita Wazamzumi. 21 Walikuwa watu wenye nguvu na wengi sana na warefu kama Waanaki;+ lakini Yehova aliwasaidia Waamoni kuwaangamiza, Waamoni wakawafukuza na kuishi humo badala yao. 22 Hivyo ndivyo alivyofanya kwa ajili ya wazao wa Esau, ambao sasa wanakaa Seiri,+ alipowaangamiza Wahori+ kutoka mbele yao, ili wamiliki nchi yao na kukaa humo badala yao mpaka leo. 23 Nao Waavi, walikuwa wakiishi katika vijiji vilivyofika Gaza,+ mpaka Wakaftori waliotoka Kaftori*+ walipokuja na kuwaangamiza na kukaa humo badala yao.)

24 “‘Ondokeni, mvuke Bonde* la Arnoni.+ Tazameni nimemtia mikononi mwenu Sihoni+ Mwamori, mfalme wa Heshboni. Basi anzeni kumiliki nchi yake, nanyi mpigane vita naye. 25 Siku ya leo nitaanza kuwafanya watu wote duniani* wanaosikia habari zenu wawahofu na kuwaogopa ninyi. Watakuwa na wasiwasi na kutetemeka* kwa sababu yenu.’+

26 “Kisha kutoka katika nyika ya Kedemothi,+ niliwatuma wajumbe kwa Mfalme Sihoni wa Heshboni, ili wampe ujumbe huu wa amani:+ 27 ‘Niruhusu nipite katika nchi yako. Nitatembea barabarani tu, sitakwenda kulia wala kushoto.+ 28 Nitakula tu chakula na kunywa tu maji utakayoniuzia. Niruhusu tu nipite kwa miguu, 29 hivyo ndivyo wazao wa Esau wanaokaa Seiri na Wamoabu wanaokaa Ari walivyonifanyia, mpaka nitakapovuka Yordani na kuingia nchi ambayo Yehova Mungu wetu anatupa sisi.’ 30 Lakini Mfalme Sihoni wa Heshboni hakuturuhusu tupite, kwa sababu Yehova Mungu wenu alimwacha awe na roho ya ukaidi+ na moyo wake uwe mgumu, ili amtie mikononi mwenu kama ilivyo leo.+

31 “Kisha Yehova akaniambia, ‘Angalieni, tayari nimeanza kumtia mikononi mwenu Sihoni pamoja na nchi yake. Anzeni kuimiliki nchi yake.’+ 32 Sihoni alipotoka na watu wake wote ili kupigana nasi kule Yahazi,+ 33 Yehova Mungu wetu alimtia mikononi mwetu, hivi kwamba tukamshinda yeye, wanawe, na watu wake wote. 34 Tuliteka majiji yake yote wakati huo na kuangamiza kila jiji, pamoja na wanaume, wanawake, na watoto. Hatukumwacha mtu yeyote akiwa hai.+ 35 Tulijichukulia tu mifugo pamoja na nyara za majiji tuliyokuwa tumeteka. 36 Kuanzia Aroeri,+ jiji lililo kwenye ukingo wa Bonde* la Arnoni (pamoja na jiji lililo bondeni), mpaka Gileadi, hakuna mji wowote ambao hatungeweza kuuteka. Yehova Mungu wetu aliitia yote mikononi mwetu.+ 37 Hata hivyo, hamkukaribia nchi ya Waamoni,+ ukingo wote wa Bonde* la Yaboki+ na majiji yaliyo kwenye eneo lenye milima, wala eneo lingine lolote tulilokatazwa na Yehova Mungu wetu.

3 “Kisha tuligeuka na kupanda kupitia njia ya Bashani. Ndipo Ogu, mfalme wa Bashani, akatoka pamoja na watu wake wote ili kupigana vita nasi kule Edrei.+ 2 Basi Yehova akaniambia, ‘Usimwogope, kwa maana nitamtia mikononi mwako pamoja na watu wake wote na nchi yake, nawe utamtendea kama ulivyomtendea Sihoni mfalme wa Waamori, aliyeishi Heshboni.’ 3 Basi Yehova Mungu wetu akamtia pia mikononi mwetu Mfalme Ogu wa Bashani pamoja na watu wake wote, nasi tukaendelea kumshambulia hivi kwamba hakuna mtu yeyote kati ya watu wake aliyeokoka. 4 Kisha tukateka majiji yake yote. Hakuna mji wao hata mmoja ambao hatukuuteka, tuliteka majiji 60 katika eneo lote la Argobu, yaani, ufalme wa Ogu kule Bashani.+ 5 Majiji hayo yote yalikuwa na kuta ndefu zenye ngome, malango, na makomeo, tuliteka pia miji mingi sana ya mashambani. 6 Hata hivyo, tuliwaangamiza,+ kama tulivyomwangamiza Mfalme Sihoni wa Heshboni, tuliangamiza kila jiji, kutia ndani wanaume, wanawake, na watoto.+ 7 Nasi tukajichukulia mifugo yote na nyara za majiji hayo.

8 “Wakati huo tulichukua nchi ya wafalme wawili wa Waamori+ waliokuwa katika eneo la Yordani, kuanzia Bonde* la Arnoni mpaka Mlima Hermoni+ 9 (Wasidoni walikuwa wakiuita mlima huo Sirioni, nao Waamori walikuwa wakiuita Seniri), 10 majiji yote yaliyokuwa katika nchi tambarare, nchi yote ya Gileadi, nchi yote ya Bashani mpaka Saleka na Edrei,+ majiji ya ufalme wa Ogu kule Bashani. 11 Kwa maana Mfalme Ogu wa Bashani ndiye Mrefaimu pekee aliyekuwa amebaki. Jeneza lake lilitengenezwa kwa chuma,* na bado liko katika jiji la Waamoni la Raba. Lina urefu wa mikono tisa* na upana wa mikono minne, kulingana na kipimo cha kawaida cha mkono. 12 Wakati huo tulimiliki nchi hii: kuanzia Aroeri,+ karibu na Bonde* la Arnoni, na nusu ya eneo lenye milima la Gileadi, na majiji yake nimewapa watu wa kabila la Rubeni na kabila la Gadi.+ 13 Kisha nusu ya kabila la Manase+ nimewapa sehemu inayobaki ya Gileadi na eneo lote la Bashani la ufalme wa Ogu. Eneo lote la Argobu, la Bashani, lilijulikana kuwa nchi ya Warefaimu.

14 “Yairi+ mwana wa Manase alichukua eneo lote la Argobu+ hadi kwenye mpaka wa Wageshuri na Wamaakathi,+ akaviita vijiji hivyo vya Bashani kwa jina lake mwenyewe, Hawoth-yairi,*+ mpaka leo. 15 Naye Makiri nimempa Gileadi.+ 16 Na watu wa kabila la Rubeni na kabila la Gadi+ nimewapa kuanzia Gileadi mpaka kwenye Bonde* la Arnoni, katikati ya bonde ulikuwa ndio mpaka, hadi Bonde la Yaboki, ambalo ni mpaka wa Waamoni, 17 na Araba na Yordani na ule mpaka, kuanzia Kinerethi hadi Bahari ya Araba, Bahari ya Chumvi, chini ya mteremko wa Pisga kuelekea upande wa mashariki.+

18 “Kisha nikawaamuru hivi: ‘Yehova Mungu wenu amewapa nchi hii mwimiliki. Wanaume wenu wote mashujaa watachukua silaha na kuvuka mbele ya ndugu zenu, Waisraeli.+ 19 Lakini wake zenu, watoto wenu, na wanyama wenu tu (najua vizuri kwamba mna wanyama wengi sana) ndio watakaoendelea kukaa katika majiji ambayo nimewapa, 20 mpaka Yehova atakapowapumzisha ndugu zenu, kama anavyowapumzisha ninyi, nao pia waimiliki nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa ng’ambo ya Yordani. Ndipo mtakaporudi, kila mmoja atarudi kwenye miliki yake ambayo nimempa.’+

21 “Wakati huo nilimwamuru hivi Yoshua:+ ‘Umeona kwa macho yako mwenyewe mambo ambayo Yehova Mungu wako amewatendea wafalme hao wawili. Hivyo ndivyo Yehova atakavyozitendea falme zote huko mnakovuka kwenda.+ 22 Msiwaogope, kwa maana Yehova Mungu wenu ndiye anayewapigania ninyi.’+

23 “Wakati huo nilimsihi hivi Yehova: 24 ‘Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, umeanza kumwonyesha mtumishi wako ukuu wako na mkono wako wenye nguvu,+ kwa maana ni mungu gani mbinguni au duniani anayetenda mambo makuu kama wewe?+ 25 Tafadhali niruhusu nivuke na kuona nchi nzuri iliyo ng’ambo ya Yordani, eneo hili zuri lenye milima na Lebanoni.’+ 26 Lakini bado Yehova alikuwa amenikasirikia vikali kwa sababu yenu,+ naye hakutaka kunisikiliza. Badala yake Yehova aliniambia, ‘Imetosha! Usizungumze nami tena kamwe kuhusu jambo hili. 27 Panda juu ya kilele cha Pisga,+ utazame magharibi na kaskazini na kusini na mashariki, uone nchi hiyo kwa macho yako, kwa maana hutavuka mto huu wa Yordani.+ 28 Nawe umweke Yoshua+ kuwa kiongozi, umtie moyo na kumwimarisha, kwa sababu yeye ndiye atakayewaongoza watu hawa kuvuka+ na kuwawezesha kuirithi nchi utakayoiona.’ 29 Mambo hayo yote yalitendeka tulipokuwa tukikaa katika bonde lililo mbele ya Beth-peori.+

4 “Sasa, enyi Waisraeli, sikilizeni masharti na sheria ambazo* ninawafundisha kushika, ili mwishi+ na kuingia kuimiliki nchi ambayo Yehova, Mungu wa mababu zenu, anawapa ninyi. 2 Hampaswi kuongeza jambo lolote kwenye neno ninalowaamuru, wala kuondoa jambo lolote kutoka katika neno hilo,+ ili mzishike amri za Yehova Mungu wenu ninazowaamuru ninyi.

3 “Macho yenu wenyewe yameona mambo ambayo Yehova alitenda kuhusiana na kisa cha Baali wa Peori; Yehova Mungu wenu alimwangamiza kila mtu miongoni mwenu aliyemfuata Baali wa Peori.+ 4 Lakini ninyi mnaoshikamana kabisa na Yehova Mungu wenu, nyote mko hai leo. 5 Tazameni, nimewafundisha masharti na sheria,*+ kama nilivyoamriwa na Yehova Mungu wangu, ili mzishike katika nchi mtakayomiliki. 6 Ni lazima mzifuate kwa uangalifu,+ kwa sababu watu watakaosikia kuhusu masharti haya yote wataona kwamba mna hekima+ na uelewaji,+ nao watasema, ‘Kwa hakika watu wa taifa hili kubwa wana hekima na uelewaji.’+ 7 Kwa maana ni taifa gani kubwa ambalo miungu yake iko karibu nalo kama Yehova Mungu wetu alivyo karibu nasi wakati wowote tunapomlilia?+ 8 Na ni taifa gani kubwa ambalo lina masharti ya uadilifu na sheria* kama Sheria hii yote ninayoweka mbele yenu leo?+

9 “Ila tu muwe waangalifu na kujihadhari sana, ili msisahau mambo ambayo macho yenu yameona na ili yasiondoke moyoni mwenu siku zote za maisha yenu. Ni lazima pia muwaambie wana wenu na wajukuu wenu.+ 10 Siku ambayo mlisimama mbele za Yehova Mungu wenu kule Horebu, Yehova aliniambia, ‘Wakusanye watu mbele zangu ili niwafanye wasikie maneno yangu,+ ili wajifunze kuniogopa+ siku zote ambazo watakuwa hai juu ya ardhi na ili wawafundishe wana wao.’+

11 “Basi mlikaribia na kusimama chini ya mlima, na mlima huo ulikuwa ukiwaka moto uliofika mpaka mbinguni; kulikuwa na giza, wingu, na utusitusi mzito.+ 12 Yehova akaanza kuzungumza nanyi kutoka katika moto.+ Mlisikia maneno, lakini hamkuona umbo lolote+—kulikuwa na sauti tu.+ 13 Naye akawatangazia agano lake,+ alilowaamuru mshike—zile Amri Kumi.*+ Kisha akaziandika kwenye mabamba mawili ya mawe.+ 14 Wakati huo, Yehova aliniamuru niwafundishe masharti na sheria ambazo * mnapaswa kushika katika nchi mtakayoingia kuimiliki.

15 “Kwa hiyo, jihadharini sana—kwa sababu hamkuona umbo lolote siku ambayo Yehova alizungumza nanyi kule Horebu kutoka katikati ya moto— 16 ili msitende upotovu kwa kujitengenezea sanamu ya kuchongwa yenye umbo la mfano wowote, mfano wa mwanamume au mwanamke,+ 17 mfano wa mnyama yeyote duniani au mfano wa ndege yeyote anayeruka angani,+ 18 mfano wa kitu chochote kinachotambaa ardhini au mfano wa samaki yeyote aliye ndani ya maji chini ya dunia.+ 19 Nanyi mnapoinua macho yenu kutazama mbinguni na kuona jua na mwezi na nyota—jeshi lote la mbinguni—msishawishiwe kuviinamia na kuviabudu.+ Yehova Mungu wenu amewapa watu wote duniani* vitu hivyo. 20 Lakini ninyi ndio watu ambao Yehova aliwatoa katika tanuru la kuyeyushia chuma, kutoka Misri, ili muwe watu ambao ni mali yake*+ mwenyewe, kama mlivyo leo.

21 “Yehova alinikasirikia kwa sababu yenu,+ akaapa kwamba sipaswi kuvuka Yordani au kuingia katika nchi nzuri ambayo Yehova Mungu wenu anawapa iwe urithi wenu.+ 22 Kwa maana nitakufa katika nchi hii; sitavuka Yordani,+ lakini ninyi mtavuka na kuimiliki nchi hiyo nzuri. 23 Iweni waangalifu msisahau agano la Yehova Mungu wenu ambalo alifanya pamoja nanyi,+ na msijitengenezee sanamu ya kuchongwa, umbo la kitu chochote mlichokatazwa na Yehova Mungu wenu.+ 24 Kwa maana Yehova Mungu wenu ni moto unaoteketeza,+ Mungu anayetaka watu wamwabudu yeye peke yake.+

25 “Ikiwa mtazaa wana na wajukuu na kuishi kwa muda mrefu nchini nanyi mtende upotovu na kutengeneza sanamu ya kuchongwa+ ya aina yoyote na kutenda uovu machoni pa Yehova Mungu wenu na hivyo kumkasirisha,+ 26 nachukua mbingu na dunia ili ziwe mashahidi dhidi yenu leo ya kwamba kwa hakika mtaangamia haraka kutoka katika nchi mnayovuka Yordani kwenda kuimiliki. Hamtaishi kwa muda mrefu katika nchi hiyo, badala yake mtaangamizwa kabisa.+ 27 Yehova atawatawanya miongoni mwa mataifa,+ na ni watu wachache tu kati yenu watakaookoka+ miongoni mwa mataifa ambayo Yehova atawafukuza ninyi mwende miongoni mwao. 28 Huko mtalazimika kuiabudu miungu ya miti na mawe iliyotengenezwa kwa mikono ya wanadamu,+ miungu ambayo haiwezi kuona wala kusikia wala kula wala kunusa.

29 “Mkimtafuta Yehova Mungu wenu mkiwa huko, hakika mtampata,+ naam, mkiutafuta ushauri wake kwa moyo wenu wote na kwa nafsi* yenu yote.+ 30 Baadaye mtakapokuwa mkiteseka sana na mambo hayo yote yatakapokuwa yamewapata, ndipo mtakapomrudia Yehova Mungu wenu na kuisikiliza sauti yake.+ 31 Kwa maana Yehova Mungu wenu ni Mungu mwenye rehema.+ Hatawaacha wala kuwaangamiza wala kusahau agano alilowaapia mababu zenu.+

32 “Sasa, ulizeni kuhusu siku za zamani kabla ya ninyi kuwepo, tangu siku ambayo Mungu alimuumba mwanadamu duniani; tafuteni kuanzia mwisho mmoja wa mbingu mpaka mwisho mwingine wa mbingu. Je, kuna jambo lolote kubwa kama hili ambalo limewahi kutokea au kuna jambo lolote kama hili ambalo limewahi kusikiwa?+ 33 Je, kuna taifa lingine lolote ambalo limewahi kusikia sauti ya Mungu ikisema kutoka katika moto kama ninyi mlivyosikia na kuendelea kuishi?+ 34 Au je, Mungu amewahi kujaribu kujichukulia taifa kutoka kati ya taifa lingine kwa hukumu,* kwa ishara, kwa miujiza,+ kwa vita,+ kwa mkono wenye nguvu,+ kwa mkono ulionyooshwa, na kwa matendo ya kutisha,+ kama Yehova Mungu wenu alivyowafanyia kule Misri mbele ya macho yenu wenyewe? 35 Ninyi wenyewe mmeonyeshwa mambo hayo ili mjue kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli;+ hakuna mwingine isipokuwa yeye.+ 36 Aliwawezesha kusikia sauti yake kutoka mbinguni ili awarekebishe, na duniani aliwawezesha kuona moto wake mkubwa, na maneno yake mliyasikia kutoka katika moto.+

37 “Kwa sababu aliwapenda mababu zenu na amechagua uzao wao* baada yao,+ naye aliwatoa Misri kwa nguvu zake kuu mbele ya macho yake. 38 Naye aliyafukuza kutoka mbele yenu mataifa makubwa zaidi na yenye nguvu zaidi kuliko ninyi, ili awalete ninyi katika nchi yao na kuwapa iwe urithi wenu, kama ilivyo leo.+ 39 Kwa hiyo, siku ya leo, mjue na kutia moyoni kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli juu mbinguni na chini duniani.+ Hakuna mwingine.+ 40 Ni lazima mshike masharti yake na amri zake ninazowapa ninyi leo, ili mambo yawaendee vyema ninyi na wana wenu baada yenu, ili mwendelee kuishi kwa muda mrefu katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa.”+

41 Wakati huo Musa alitenga majiji matatu upande wa mashariki wa Yordani.+ 42 Mtu yeyote anayemuua mwenzake bila kukusudia na hakuwa akimchukia,+ ni lazima akimbilie katika mojawapo ya majiji hayo ili aishi.+ 43 Majiji hayo ni Beseri+ kule nyikani katika uwanda wa juu kwa ajili ya watu wa kabila la Rubeni, Ramothi+ kule Gileadi kwa ajili ya watu wa kabila la Gadi, na Golani+ kule Bashani kwa ajili ya watu wa kabila la Manase.+

44 Basi hiyo ndiyo Sheria+ ambayo Musa aliwapa Waisraeli. 45 Hivyo ndivyo vikumbusho, masharti, na sheria ambazo* Musa aliwapa Waisraeli baada ya kutoka Misri,+ 46 katika eneo la Yordani, kwenye bonde lililo ng’ambo ya Beth-peori,+ katika nchi ya Mfalme Sihoni wa Waamori, aliyekuwa akikaa Heshboni,+ ambaye Musa na Waisraeli walimshinda walipotoka Misri.+ 47 Nao wakaimiliki nchi yake na nchi ya Mfalme Ogu+ wa Bashani, wafalme wawili wa Waamori waliokuwa katika eneo lililokuwa upande wa mashariki wa Yordani, 48 kuanzia Aroeri,+ kwenye ukingo wa Bonde la Arnoni, mpaka Mlima Sioni, yaani, Hermoni,+ 49 na eneo lote la Araba upande wa mashariki wa Yordani, mpaka Bahari ya Araba,* chini ya miteremko ya Pisga.+

5 Kisha Musa akawaita Waisraeli wote na kuwaambia hivi: “Enyi Waisraeli, sikilizeni masharti na sheria ambazo* ninawatangazia ninyi leo, nanyi mnapaswa kujifunza na kushika kwa uangalifu masharti na sheria hizo. 2 Yehova Mungu wetu alifanya agano pamoja nasi kule Horebu.+ 3 Yehova hakufanya agano hilo pamoja na mababu zetu, bali pamoja nasi, sisi sote tulio hai hapa leo. 4 Yehova alizungumza nanyi uso kwa uso mlimani, kutoka katika moto.+ 5 Wakati huo nilisimama kati yenu na Yehova+ ili niwaambie neno la Yehova, kwa maana mliogopa kwa sababu ya moto nanyi hamkupanda mlimani.+ Alisema hivi:

6 “‘Mimi ni Yehova Mungu wako, niliyekutoa katika nchi ya Misri, kutoka katika nyumba ya utumwa.+ 7 Hupaswi kamwe kuwa na miungu mingine ila mimi.*+

8 “‘Usijitengenezee sanamu ya kuchongwa+ au mfano wa* kitu chochote kilicho juu mbinguni au kilicho chini duniani au kilicho ndani ya maji chini ya dunia. 9 Usiviinamie wala kushawishiwa kuviabudu,+ kwa sababu mimi, Yehova Mungu wako, ni Mungu ninayetaka watu waniabudu mimi peke yangu,+ nami huwaadhibu watoto kwa sababu ya makosa ya baba zao, kufikia kizazi cha tatu na kizazi cha nne cha wale wanaonichukia,+ 10 lakini ninawatendea kwa upendo mshikamanifu* watu wanaonipenda na kushika amri zangu, kufikia kizazi chao cha elfu.

11 “‘Usilitumie jina langu mimi, Yehova Mungu wako, kwa njia isiyofaa,+ kwa maana mimi Yehova sitakosa kumwadhibu yule anayelitumia jina langu kwa njia isiyofaa.+

12 “‘Ishike siku ya Sabato na uione kuwa takatifu, kama mimi Yehova Mungu wako nilivyokuamuru.+ 13 Fanya shughuli na kazi zako zote kwa siku sita,+ 14 lakini siku ya saba ni sabato kwa Yehova Mungu wako.+ Usifanye kazi yoyote,+ wewe, wala mwana wako, wala binti yako, wala mtumwa wako, wala kijakazi wako, wala ng’ombe dume wako, wala punda wako, wala mnyama yeyote unayemfuga, wala mgeni anayekaa katika majiji*+ yenu, ili mtumwa wako na kijakazi wako wapumzike kama wewe.+ 15 Kumbuka kwamba ulikuwa mtumwa nchini Misri, na mimi Yehova Mungu wako nikakutoa huko kwa mkono wenye nguvu na mkono ulionyooshwa.+ Ndiyo sababu mimi Yehova Mungu wako nilikuamuru uishike siku ya Sabato.

16 “‘Mheshimu baba yako na mama yako,+ kama mimi Yehova Mungu wako nilivyokuamuru, ili uishi muda mrefu na kufanikiwa* katika nchi ambayo mimi Yehova Mungu wako ninakupa.+

17 “‘Usiue.+

18 “‘Wala usifanye uzinzi.+

19 “‘Wala usiibe.+

20 “‘Wala usitoe ushahidi wa uwongo dhidi ya jirani yako.+

21 “‘Wala usimtamani mke wa jirani yako.+ Wala usitamani kwa ubinafsi nyumba ya jirani yako, wala shamba lake, wala mtumwa wake, wala kijakazi wake, wala ng’ombe dume wake, wala punda wake, wala kitu chochote cha jirani yako.’+

22 “Yehova aliwapa amri hizo* ninyi nyote mlimani, kutoka katika moto, wingu, na utusitusi mzito,+ kwa sauti kubwa, naye hakuongeza lolote; kisha akaziandika kwenye mabamba mawili ya mawe na kunipa.+

23 “Lakini mara tu mliposikia sauti kutoka katika lile giza, mlima ulipokuwa ukiwaka moto,+ viongozi wote wa makabila yenu na wazee wakanijia. 24 Kisha mkasema, ‘Tazama, Yehova Mungu wetu ametuonyesha utukufu wake na ukuu wake, nasi tumesikia sauti yake kutoka katika moto.+ Leo tumeona kwamba Mungu anaweza kuongea na mwanadamu na mwanadamu huyo aendelee kuishi.+ 25 Sasa, kwa nini tufe? Kwa maana moto huu mkubwa unaweza kututeketeza. Tukiendelea kuisikia sauti ya Yehova Mungu wetu, hakika tutakufa. 26 Kwa maana ni nani kati ya wanadamu wote* aliyesikia sauti ya Mungu aliye hai ikiongea kutoka katika moto kama tulivyosikia na bado anaishi? 27 Wewe mwenyewe nenda karibu, usikie yote ambayo Yehova Mungu wetu atasema, nawe ndiwe utakayetuambia mambo yote ambayo Yehova Mungu wetu anakuambia, nasi tutasikiliza na kutenda mambo hayo.’+

28 “Basi Yehova alisikia maneno mliyoniambia, naye Yehova akaniambia, ‘Nimesikia maneno ambayo watu hawa wamekuambia. Mambo yote waliyosema ni sawa.+ 29 Laiti sikuzote wangekuwa na moyo wenye mwelekeo wa kuniogopa+ na kushika amri zangu zote;+ basi mambo yangewaendea vyema wao na wana wao milele!+ 30 Nenda uwaambie hivi: “Rudini kwenye mahema yenu.” 31 Lakini unapaswa kubaki hapa pamoja nami, nami nitakuambia amri zote, masharti, na sheria unazopaswa kuwafundisha na ambazo wanapaswa kushika katika nchi ninayowapa wamiliki.’ 32 Sasa ninyi watu mnapaswa kuwa waangalifu kufanya kama Yehova Mungu wenu alivyowaamuru.+ Msigeuke kwenda kulia wala kushoto.+ 33 Mnapaswa kutembea katika njia yote ambayo Yehova Mungu wenu amewaamuru mfuate,+ ili mwishi na kufanikiwa na kurefusha siku zenu katika nchi mtakayomiliki.+

6 “Sasa hizi ndizo amri, masharti, na sheria ambazo Yehova Mungu wako ametoa ili ufundishwe, ili uzishike unapovuka kuingia katika nchi ambayo utaimiliki, 2 ili umwogope Yehova Mungu wako na kushika sheria zake zote na amri zake ambazo ninakuamuru wewe—wewe na mwana wako na mjukuu wako+—siku zote za maisha yako, ili uishi muda mrefu.+ 3 Sikilizeni, enyi Waisraeli, na mzishike kwa uangalifu, ili mfanikiwe na kuwa wengi sana katika nchi inayotiririka maziwa na asali, kama Yehova, Mungu wa mababu zenu, alivyowaahidi.

4 “Sikilizeni, enyi Waisraeli: Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja.+ 5 Ni lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi*+ yako yote na kwa nguvu zako zote.*+ 6 Maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako, 7 nawe lazima uyakazie* kwa wanao+ na kuongea kuyahusu unapoketi nyumbani mwako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.+ 8 Yafunge yawe kumbukumbu mkononi mwako, na lazima yawe kama utepe kwenye paji la uso wako.*+ 9 Yaandike kwenye miimo ya milango ya nyumba yako na kwenye malango yako.

10 “Yehova Mungu wenu atakapowaleta katika nchi aliyowaapia mababu zenu Abrahamu, Isaka, na Yakobo kwamba atawapa ninyi+—majiji makubwa na yenye kupendeza ambayo hamkujenga,+ 11 nyumba zilizojaa vitu vizuri vya aina mbalimbali ambavyo hamkufanya kazi ili kuvipata, visima ambavyo hamkuchimba, na mashamba ya mizabibu na mizeituni ambayo hamkupanda—nanyi mtakapokuwa mmekula na kushiba,+ 12 jihadharini msimsahau Yehova,+ aliyewatoa nchini Misri, kutoka katika nyumba ya utumwa. 13 Mnapaswa kumwogopa+ Yehova Mungu wenu, mnapaswa kumtumikia yeye,+ nanyi mnapaswa kuapa kwa jina lake.+ 14 Msifuate miungu mingine, miungu yoyote ya mataifa yote yanayowazunguka,+ 15 kwa maana Yehova Mungu wenu ambaye yuko miongoni mwenu ni Mungu anayetaka watu wamwabudu yeye peke yake.+ Msipofanya hivyo, hasira ya Yehova Mungu wenu itawaka dhidi yenu,+ naye atawaangamiza kabisa kutoka duniani.+

16 “Msimjaribu Yehova Mungu wenu kama mlivyomjaribu+ kule Masa.+ 17 Mnapaswa kuzishika kwa bidii amri za Yehova Mungu wenu na vikumbusho vyake na masharti yake ambayo amewaamuru mshike. 18 Ni lazima mfanye mambo mema na yanayofaa machoni pa Yehova, ili mfanikiwe na ili mwingie na kuimiliki nchi nzuri ambayo Yehova aliwaapia mababu zenu,+ 19 kwa kuwafukuza maadui wenu wote kutoka mbele yenu, kama Yehova alivyoahidi.+

20 “Wakati ujao, mwana wako akikuuliza, ‘Vikumbusho, masharti, na sheria* ambazo Yehova Mungu wetu ametuamuru tushike zinamaanisha nini?’ 21 ndipo utakapomwambia mwana wako, ‘Tulikuwa watumwa wa Farao kule Misri, lakini Yehova alitutoa Misri kwa mkono wenye nguvu. 22 Basi mbele ya macho yetu, Yehova aliendelea kufanya ishara na miujiza mikubwa na iliyoleta uharibifu nchini Misri,+ na pia kwa Farao na nyumba yake yote.+ 23 Naye akatutoa huko ili atulete hapa na kutupatia nchi ambayo aliwaapia mababu zetu.+ 24 Kisha Yehova akatuamuru tufuate masharti hayo yote na kumwogopa Yehova Mungu wetu ili tufanikiwe daima,+ na ili tuendelee kuishi,+ kama ilivyo leo. 25 Tukimtii Yehova Mungu wetu kwa kushika kwa uangalifu amri hizo zote, kama alivyotuamuru, tutakuwa waadilifu.’+

7 “Yehova Mungu wenu atakapowaleta katika nchi mnayokaribia kuingia na kuimiliki,+ atayaondoa pia mataifa makubwa kutoka mbele yenu:+ Wahiti, Wagirgashi, Waamori,+ Wakanaani, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi,+ mataifa saba makubwa zaidi na yenye nguvu kuliko ninyi.+ 2 Yehova Mungu wenu atawatia watu hao mikononi mwenu, nanyi mtawashinda.+ Mnapaswa kuwaangamiza kabisa.+ Msifanye agano lolote pamoja nao wala kuwahurumia.+ 3 Msioane nao kamwe. Msikubali mabinti wenu waolewe na wana wao wala msikubali wana wenu wawaoe mabinti wao.+ 4 Kwa maana watawapotosha wana wenu waache kumfuata Mungu na kuanza kuabudu miungu mingine;+ kisha hasira ya Yehova itawaka dhidi yenu, naye atawaangamiza upesi.+

5 “Lakini hivi ndivyo mtakavyowatendea: Bomoeni madhabahu zao, vunjeni nguzo zao takatifu,+ kateni miti yao mitakatifu,*+ na kuteketeza sanamu zao za kuchongwa.+ 6 Kwa maana ninyi ni watu watakatifu kwa Yehova Mungu wenu, na Yehova Mungu wenu amewachagua ninyi muwe watu wake, mali yake ya pekee,* kutoka kati ya mataifa yote yaliyo duniani.+

7 “Yehova hakuwapenda na kuwachagua ninyi eti kwa sababu mlikuwa wengi kuliko mataifa yote,+ kwa maana mlikuwa taifa dogo zaidi kati ya mataifa yote.+ 8 Badala yake, ni kwa sababu Yehova anawapenda na alitimiza kiapo alichowaapia mababu zenu,+ ndiyo maana Yehova aliwatoa Misri kwa mkono wake wenye nguvu na kuwakomboa kutoka katika nyumba ya utumwa,+ kutoka katika nguvu za* Farao mfalme wa Misri. 9 Mnajua vizuri kwamba Yehova Mungu wenu ndiye Mungu wa kweli, Mungu mwaminifu, anayetimiza agano lake na kutenda kwa upendo mshikamanifu kufikia kizazi cha elfu cha wale wanaompenda na kushika amri zake.+ 10 Lakini wale wanaomchukia atawalipa waziwazi* kwa kuwaangamiza.+ Hatakawia kuwaadhibu wale wanaomchukia; atawalipa waziwazi.* 11 Kwa hiyo, muwe waangalifu kushika amri na masharti na sheria ambazo* ninawaamuru leo, kwa kuzifuata.

12 “Mkiendelea kusikiliza sheria hizi na kuzifuata na kuzitekeleza, Yehova Mungu wenu atatimiza lile agano na kuwatendea kwa upendo mshikamanifu kama alivyowaapia mababu zenu. 13 Atawapenda na kuwabariki na kuwafanya mwongezeke. Naam, atawabariki kwa kuwapa watoto wengi,*+ mazao ya ardhi yenu, nafaka yenu, divai yenu mpya, mafuta yenu,+ ndama na wanakondoo wa makundi yenu, katika nchi aliyowaapia mababu zenu kwamba atawapa ninyi.+ 14 Mtabarikiwa kuliko mataifa mengine yote;+ hakuna mwanamume au mwanamke yeyote miongoni mwenu atakayekosa mtoto, wala mifugo yenu haitakosa kuzaa.+ 15 Yehova atawaondolea magonjwa yote, naye hatawaletea ugonjwa wowote unaotisha mlioujua kule Misri.+ Badala yake, atawaletea magonjwa hayo wote wanaomchukia. 16 Mtayaangamiza* mataifa yote ambayo Yehova Mungu wenu atayatia mikononi mwenu.+ Msiwahurumie*+ kamwe, nanyi msiabudu kamwe miungu yao,+ kwa sababu jambo hilo litakuwa mtego kwenu.+

17 “Mkijiambia mioyoni mwenu, ‘Mataifa haya yana watu wengi kuliko sisi. Tunawezaje kuyafukuza?’+ 18 msiwaogope.+ Mnapaswa kujikumbusha mambo ambayo Yehova Mungu wenu alimtendea Farao na nchi yote ya Misri,+ 19 zile hukumu kubwa* ambazo mliona kwa macho yenu na ishara na miujiza+ na mkono wenye nguvu na mkono ulionyooshwa ambao Yehova Mungu wenu aliutumia kuwatoa huko.+ Hivyo ndivyo Yehova Mungu wenu atakavyoyatendea mataifa yote mnayoyaogopa.+ 20 Yehova Mungu wenu atawafanya wavunjike moyo* mpaka watakapoangamia wale waliobaki+ na waliokuwa wakijificha ili msiwapate. 21 Msishtuke kwa sababu yao, kwa maana Yehova Mungu wenu yuko pamoja nanyi,+ Mungu mkuu na mwenye kuogopesha.+

22 “Kwa hakika Yehova Mungu wenu atayafukuza mataifa haya kutoka mbele yenu kidogo kidogo.+ Hamtaruhusiwa kuwaangamiza upesi, ili wanyama wa mwituni wasiongezeke na kuwashambulia ninyi. 23 Yehova Mungu wenu atayatia mikononi mwenu na kuyashinda kabisa mpaka yaangamie.+ 24 Atawatia wafalme wa mataifa hayo mikononi mwenu,+ nanyi mtayafutilia mbali majina yao kutoka duniani.*+ Hakuna mtu atakayewazuia,+ mpaka mtakapowaangamiza.+ 25 Mnapaswa kuchoma moto sanamu za kuchongwa za miungu yao.+ Msitamani fedha na dhahabu ya sanamu hizo wala msiichukue,+ ili isiwe mtego kwenu, kwa maana ni chukizo kwa Yehova Mungu wenu.+ 26 Msilete ndani ya nyumba zenu kitu kinachochukiza kwa sababu mtakuwa kama kitu hicho kinachopaswa kuharibiwa. Mnapaswa kukichukia kabisa na kukikirihi kabisa, kwa sababu ni kitu kinachopaswa kuharibiwa.

8 “Mnapaswa kuwa waangalifu kushika kila amri ninayowapa leo, ili mwendelee kuishi, mwongezeke,+ mwingie na kuimiliki nchi ambayo Yehova aliwaapia mababu zenu.+ 2 Kumbukeni njia ndefu ambayo Yehova Mungu wenu alifanya mtembee nyikani kwa miaka hii 40,+ ili awanyenyekeze na kuwajaribu+ ili ajue yaliyokuwa mioyoni mwenu,+ aone kama mngezishika amri zake au la. 3 Kwa hiyo aliwanyenyekeza na kuwaacha mkae njaa,+ naye akawalisha mana,+ ambayo ninyi wala baba zenu hamkuwa mmeijua, ili awafundishe kwamba mwanadamu haishi kwa mkate tu bali huishi kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.+ 4 Nguo mlizovaa hazikuchakaa, wala miguu yenu haikuvimba miaka hiyo 40.+ 5 Mnajua vizuri mioyoni mwenu kwamba kama baba anavyomrekebisha mwana wake, ndivyo Yehova Mungu wenu alivyokuwa akiwarekebisha.+

6 “Basi ni lazima mshike amri za Yehova Mungu wenu kwa kutembea katika njia zake na kumwogopa yeye. 7 Kwa maana Yehova Mungu wenu anawaleta katika nchi nzuri,+ nchi yenye vijito vya maji, mabubujiko na chemchemi zinazotiririka* katika bonde tambarare na katika eneo lenye milima, 8 nchi yenye ngano na shayiri, na mizabibu, mitini, na mikomamanga,+ nchi yenye mafuta ya zeituni na asali,+ 9 nchi ambayo haitakuwa na upungufu wa chakula na hamtakosa chochote, nchi yenye mawe yaliyo na chuma na katika milima yake mtachimba shaba.

10 “Baada ya kula na kushiba, mnapaswa kumsifu Yehova Mungu wenu kwa sababu ya nchi nzuri ambayo amewapa.+ 11 Jihadharini msimsahau Yehova Mungu wenu kwa kutoshika amri zake, maagizo yake, na sheria zake ambazo ninawaamuru leo. 12 Baada ya kula na kushiba na kujenga nyumba nzuri na kukaa humo,+ 13 ng’ombe wenu na kondoo wenu watakapokuwa wameongezeka na fedha yenu na dhahabu yenu itakapokuwa imeongezeka na mtakapokuwa na wingi wa vitu vyote, 14 msiache mioyo yenu iwe na kiburi+ na kuwafanya mumsahau Yehova Mungu wenu, aliyewatoa nchini Misri, kutoka katika nyumba ya utumwa,+ 15 aliyewafanya mtembee katika nyika kubwa na yenye kutisha,+ iliyo na nyoka wenye sumu na nge na ardhi iliyokauka isiyo na maji. Alifanya maji yatiririke kutoka katika mwamba mgumu+ 16 na kuwalisha mana+ nyikani, ambayo baba zenu hawakuwa wameijua, ili awanyenyekeze+ na kuwajaribu ili awanufaishe baadaye.+ 17 Mkijiambia mioyoni mwenu, ‘Nimepata utajiri huu kwa nguvu zangu mwenyewe na uwezo wa mkono wangu mwenyewe,’+ 18 kumbukeni kwamba Yehova Mungu wenu ndiye anayewapa nguvu za kupata utajiri,+ ili atimize agano lake ambalo aliwaapia mababu zenu, kama ilivyo leo.+

19 “Ikiwa mtamsahau Yehova Mungu wenu na kufuata miungu mingine na kuiabudu na kuiinamia, nashuhudia dhidi yenu leo kwamba hakika mtaangamia.+ 20 Mtaangamia kama mataifa ambayo Yehova anayaangamiza mbele yenu, kwa sababu hamkuisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu.+

9 “Sikilizeni, enyi Waisraeli, leo mnavuka Yordani+ na kuingia kumiliki nchi yenye mataifa makubwa zaidi na yenye nguvu zaidi kuliko ninyi,+ majiji makubwa na yenye ngome zinazofika mbinguni,*+ 2 watu wenye nguvu na warefu, wana wa Waanaki,+ mnaowajua na ambao mmesikia watu wakisema hivi kuwahusu: ‘Ni nani anayeweza kuwashinda wana wa Anaki?’ 3 Kwa hiyo, mnapaswa kujua leo kwamba Yehova Mungu wenu atawatangulia mnapovuka.+ Yeye ni moto unaoteketeza,+ atawaangamiza. Atawashinda mbele ya macho yenu ili mwafukuze* na kuwaangamiza haraka, kama Yehova alivyoahidi.+

4 “Yehova Mungu wenu atakapowafukuza kutoka mbele yenu, msiseme hivi mioyoni mwenu: ‘Yehova amenileta ili nimiliki nchi hii kwa sababu ya uadilifu wangu mwenyewe.’+ Badala yake, Yehova anayafukuza mataifa hayo+ kutoka mbele yenu kwa sababu ya uovu wao. 5 Hamwendi kumiliki nchi yao kwa sababu ya uadilifu wenu au unyoofu wa mioyo yenu. Badala yake, Yehova Mungu wenu anayafukuza mataifa hayo kutoka mbele yenu+ kwa sababu ya uovu wao na ili Yehova atimize neno alilowaapia mababu zenu, Abrahamu,+ Isaka,+ na Yakobo.+ 6 Basi, mjue kwamba Yehova Mungu wenu hawapi nchi hii nzuri mwimiliki kwa sababu ya uadilifu wenu; kwa maana ninyi ni watu wakaidi.*+

7 “Kumbukeni, msisahau kamwe jinsi mlivyomkasirisha Yehova Mungu wenu nyikani.+ Tangu siku mliyotoka nchini Misri mpaka mlipofika mahali hapa, mmekuwa mkimwasi Yehova.+ 8 Hata kule Horebu mlimkasirisha Yehova, na Yehova akapandwa na hasira sana hivi kwamba alitaka kuwaangamiza.+ 9 Nilipopanda mlimani ili kupokea yale mabamba ya mawe,+ mabamba ya agano ambalo Yehova alifanya pamoja nanyi,+ nilikaa mlimani siku 40 mchana na usiku,+ sikula chakula wala kunywa maji. 10 Kisha Yehova akanipa yale mabamba mawili ya mawe yaliyoandikwa kwa kidole cha Mungu, nayo yalikuwa na maneno yote ambayo Yehova aliwaambia mlimani kutoka katika moto siku ya kusanyiko.*+ 11 Mwishoni mwa zile siku 40 mchana na usiku, Yehova alinipa yale mabamba mawili ya mawe, yale mabamba ya agano, 12 na Yehova akaniambia, ‘Ondoka, shuka upesi kutoka hapa, kwa sababu watu wako uliowatoa Misri wametenda mambo mapotovu.+ Wamegeuka upesi kutoka katika njia niliyowaamuru wafuate. Wamejitengenezea sanamu ya chuma.’*+ 13 Kisha Yehova akaniambia, ‘Nimewatazama watu hawa, nikaona ni watu wakaidi.*+ 14 Niache, nami nitawaangamiza na kufutilia mbali jina lao kutoka duniani,* na acha nikufanye wewe kuwa taifa lenye nguvu zaidi na lenye watu wengi kuliko wao.’+

15 “Basi nikageuka na kushuka mlimani huku mlima ukiwaka moto,+ nami nilikuwa nimebeba yale mabamba mawili ya agano kwa mikono yangu miwili.+ 16 Kisha nikatazama na kuona kwamba mlikuwa mmemtendea dhambi Yehova Mungu wenu! Mlikuwa mmejitengenezea ndama wa chuma.* Mlikuwa mmegeuka upesi kutoka katika njia ambayo Yehova alikuwa amewaamuru mfuate.+ 17 Basi nikashika yale mabamba mawili na kuyatupa chini kwa mikono yangu miwili na kuyavunja mbele ya macho yenu.+ 18 Kisha nikalala kifudifudi mbele za Yehova kwa siku 40, mchana na usiku, kama nilivyofanya mwanzoni. Sikula chakula wala kunywa maji,+ kwa sababu ya dhambi zote mlizokuwa mmetenda kwa kufanya uovu machoni pa Yehova na kumkasirisha. 19 Kwa maana niliogopa sana kwa sababu Yehova alikuwa amewakasirikia sana,+ naye alitaka kuwaangamiza. Hata hivyo, Yehova alinisikiliza wakati huo pia.+

20 “Yehova alimkasirikia sana Haruni hivi kwamba alitaka kumwangamiza,+ lakini wakati huo niliomba dua kwa ajili ya Haruni pia. 21 Halafu nikachukua kile kitu cha dhambi mlichokitengeneza, yule ndama,+ na kumteketeza kwa moto; nikamponda na kumsagasaga kabisa mpaka akawa laini kama mavumbi, nami nikayatupa mavumbi hayo katika kijito kinachotiririka kutoka mlimani.+

22 “Pia, mlimkasirisha Yehova kule Tabera,+ kule Masa,+ na Kibroth-hataava.+ 23 Yehova alipowatuma kutoka Kadesh-barnea+ na kuwaambia, ‘Pandeni mwimiliki nchi ambayo kwa hakika nitawapa!’ mliasi tena agizo la Yehova Mungu wenu,+ nanyi hamkuonyesha imani+ kumwelekea wala hamkumtii. 24 Mmekuwa mkimwasi Yehova tangu nilipowajua.

25 “Kwa hiyo niliendelea kulala kifudifudi mbele za Yehova siku 40, mchana na usiku,+ nililala kifudifudi kwa sababu Yehova alisema atawaangamiza. 26 Nikaanza kutoa dua kwa Yehova na kusema, ‘Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, usiwaangamize watu hawa. Wao ni mali yako binafsi,*+ watu uliowakomboa kwa ukuu wako na kuwatoa Misri kwa mkono wenye nguvu.+ 27 Wakumbuke watumishi wako Abrahamu, Isaka, na Yakobo.+ Usikazie fikira ukaidi wa watu hawa, uovu wao, na dhambi yao.+ 28 Kama sivyo watu wa nchi ulimotutoa huenda wakasema: “Yehova alishindwa kuwaingiza katika nchi aliyowaahidi, na kwa sababu aliwachukia, aliwatoa ili awaue nyikani.”+ 29 Kwa maana ni watu wako na mali yako binafsi,*+ watu uliowatoa kwa nguvu zako kuu na kwa mkono wako ulionyooshwa.’+

10 “Wakati huo Yehova aliniambia, ‘Jichongee mabamba mawili ya mawe kama yale ya kwanza,+ upande uje kwangu mlimani; jitengenezee pia sanduku la mbao. 2 Nami nitaandika kwenye mabamba hayo maneno yaliyokuwa kwenye yale mabamba ya kwanza ambayo uliyavunja, na uweke mabamba hayo ndani ya sanduku hilo.’ 3 Kwa hiyo nikatengeneza sanduku kwa mbao za mshita na kuchonga mabamba mawili ya mawe kama yale ya kwanza na kupanda juu mlimani nikiwa nimebeba mabamba hayo mawili mkononi mwangu.+ 4 Kisha akaandika kwenye mabamba hayo maneno aliyoandika mwanzoni,+ zile Amri Kumi,*+ ambazo Yehova aliwaambia mlimani kutoka katika moto+ siku ya kusanyiko;*+ Yehova akanipa mabamba hayo. 5 Basi nikageuka na kushuka kutoka mlimani+ na kuyaweka mabamba hayo katika sanduku nililokuwa nimetengeneza, na yangali humo, kama Yehova alivyokuwa ameniamuru.

6 “Kisha Waisraeli wakaondoka Beerothi Bene-yaakani na kwenda Mosera. Haruni akafa na kuzikwa huko,+ na Eleazari mwana wake akaanza kutumikia akiwa kuhani baada yake.+ 7 Kutoka huko wakaelekea Gudgoda, na kutoka Gudgoda wakaelekea Yotbata,+ nchi yenye vijito vingi vya maji.

8 “Wakati huo Yehova aliliteua kabila la Lawi+ ili libebe sanduku la agano la Yehova,+ lisimame mbele za Yehova ili kumhudumia, na kubariki katika jina lake,+ kama linavyofanya mpaka leo. 9 Ndio maana Lawi hana fungu wala urithi pamoja na ndugu zake. Yehova ndiye urithi wake, kama Yehova Mungu wako alivyokuwa amemwambia.+ 10 Mimi mwenyewe nilikaa mlimani siku 40, mchana na usiku,+ kama nilivyofanya mwanzoni, na Yehova alinisikiliza wakati huo pia.+ Yehova hakutaka kuwaangamiza. 11 Kisha Yehova akaniambia, ‘Tangulia mbele ya watu, na mjitayarishe kuondoka, ili waingie na kuimiliki nchi ambayo nimewaapia mababu zao kwamba nitawapa.’+

12 “Sasa, enyi Waisraeli, Yehova Mungu wenu anataka mfanye nini?+ Hili tu ndilo analotaka: mmwogope Yehova Mungu wenu,+ mtembee katika njia zake zote,+ mumpende, na kumtumikia Yehova Mungu wenu kwa moyo wenu wote na kwa nafsi* yenu yote,+ 13 na kushika amri na sheria za Yehova ninazowaamuru leo kwa faida yenu wenyewe.+ 14 Tazameni, mbingu, hata mbingu za mbingu* ni mali ya Yehova Mungu wenu, pamoja na dunia na vitu vyote vilivyomo.+ 15 Lakini Yehova aliwakaribia na kudhihirisha upendo wake kwa mababu zenu tu, naye amewachagua ninyi, wazao wao,+ kutoka kati ya mataifa yote, kama mlivyo leo. 16 Ni lazima sasa msafishe*+ mioyo yenu na kuacha ukaidi.*+ 17 Kwa maana Yehova Mungu wenu ni Mungu wa miungu+ na Bwana wa mabwana, Mungu mkuu, mwenye nguvu, na mwenye kuogopesha, asiyempendelea yeyote+ na hakubali rushwa. 18 Hutekeleza haki kwa ajili ya yatima na mjane+ na kumpenda mkaaji mgeni,+ humpa chakula na mavazi. 19 Ni lazima ninyi pia mumpende mkaaji mgeni, kwa maana mlikuwa wakaaji wageni katika nchi ya Misri.+

20 “Mnapaswa kumwogopa Yehova Mungu wenu, na kumtumikia yeye,+ mnapaswa kushikamana naye, nanyi mnapaswa kuapa kwa jina lake. 21 Yeye Ndiye mnayepaswa kumsifu.+ Yeye ni Mungu wenu, ambaye amewafanyia mambo haya makuu na yenye kuogopesha mliyoyaona kwa macho yenu wenyewe.+ 22 Mababu zenu waliposhuka kwenda Misri walikuwa watu* 70,+ na sasa Yehova Mungu wenu amewafanya muwe wengi kama nyota za mbinguni.+

11 “Ni lazima mumpende Yehova Mungu wenu+ na kutimiza sikuzote wajibu wenu kwake, sheria zake, maagizo yake, na amri zake. 2 Mnajua kwamba leo ninazungumza nanyi, si na wana wenu ambao hawajajua wala kuona nidhamu ya Yehova Mungu wenu,+ ukuu wake,+ mkono wake wenye nguvu+ na mkono wake ulionyooshwa. 3 Hawakuona ishara zake na matendo yake aliyotenda Misri kwa Farao mfalme wa Misri na kwa nchi yake yote;+ 4 wala mambo aliyoyatendea majeshi ya Misri, farasi wa Farao na magari yake ya vita, ambayo yalifunikwa na maji ya Bahari Nyekundu walipokuwa wakiwafuatia ninyi, na Yehova akawaangamiza milele.*+ 5 Hawakuona mambo aliyowatendea nyikani mpaka mlipofika mahali hapa, 6 wala mambo aliyowatendea Dathani na Abiramu, wana wa Eliabu mwana wa Rubeni, dunia ilipofunguka na kuwameza wao pamoja na familia zao na mahema yao na kila kiumbe aliye hai aliyewafuata, mbele ya macho ya Waisraeli wote.+ 7 Macho yenu wenyewe yameona matendo yote makuu ambayo Yehova alifanya.

8 “Ni lazima mshike amri yote ninayowapa leo, ili muwe imara na kuvuka ili kuimiliki nchi, 9 na ili mwishi muda mrefu+ katika nchi ambayo Yehova aliapa kwamba angewapa mababu zenu na uzao wao,*+ nchi inayotiririka maziwa na asali.+

10 “Nchi mnayoenda kumiliki si kama nchi ya Misri mlikotoka, ambako mlikuwa mkipanda mbegu zenu na kuzimwagilia maji kwa mguu wenu,* kama bustani ya mboga. 11 Lakini nchi mnayokaribia kuvuka kuingia humo ili kuimiliki ni nchi yenye milima na mabonde tambarare.+ Inanyweshwa na maji ya mvua kutoka mbinguni;+ 12 ni nchi inayotunzwa na Yehova Mungu wenu. Macho ya Yehova Mungu wenu yanaitazama daima, kuanzia mwanzo wa mwaka mpaka mwisho wa mwaka.

13 “Na ikiwa mtatii kwa bidii amri zangu ninazowaamuru leo na kumpenda Yehova Mungu wenu na kumtumikia kwa moyo wenu wote na kwa nafsi* yenu yote,+ 14 nitawapa* pia mvua kwa ajili ya nchi yenu katika majira yake, mvua ya vuli na mvua ya masika, nanyi mtakusanya nafaka yenu na divai yenu mpya na mafuta yenu.+ 15 Nami nitaotesha majani katika mashamba yenu kwa ajili ya mifugo yenu, nanyi mtakula na kushiba.+ 16 Jihadharini msiruhusu mioyo yenu ishawishiwe kukengeuka na kuabudu miungu mingine na kuiinamia.+ 17 Kama sivyo, hasira ya Yehova itawaka dhidi yenu, naye atafunga mbingu hivi kwamba mvua haitanyesha+ na ardhi haitazaa mazao yake nanyi mtaangamia upesi kutoka katika nchi nzuri ambayo Yehova anawapa ninyi.+

18 “Ni lazima uyakazie maneno haya yangu katika moyo wako na nafsi* yako na kuyafunga kama kumbukumbu kwenye mkono wako, nayo yanapaswa kuwa kama utepe kwenye paji la uso wako.*+ 19 Wafundishe watoto wako maneno haya, na kuongea kuyahusu unapoketi nyumbani mwako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.+ 20 Yaandike kwenye miimo ya milango ya nyumba yako na kwenye malango yako, 21 ili wewe na wana wako mwishi muda mrefu+ katika nchi ambayo Yehova aliapa kwamba angewapa mababu zenu,+ sikuzote ambazo mbingu zitakuwa juu ya dunia.

22 “Ikiwa mtaishika kabisa amri hii ninayowapa na kuitekeleza, mkimpenda Yehova Mungu wenu,+ mkitembea katika njia zake zote na kushikamana naye,+ 23 Yehova atayafukuza mataifa haya yote kutoka mbele yenu,+ nanyi mtamiliki nchi ya mataifa makubwa zaidi na yenye watu wengi kuliko ninyi.+ 24 Kila mahali mtakapokanyaga kwa mguu wenu patakuwa penu.+ Mpaka wenu utaanzia nyikani mpaka Lebanoni, kuanzia ule Mto, mto Efrati, mpaka bahari ya magharibi.*+ 25 Hakuna yeyote atakayewazuia.+ Yehova Mungu wenu atawafanya wakaaji wote wa nchi mtakayokanyaga wawahofu na kuwaogopa,+ kama alivyowaahidi ninyi.

26 “Tazameni, leo ninaweka mbele yenu baraka na laana:+ 27 baraka, ikiwa mtatii amri za Yehova Mungu wenu ninazowaamuru ninyi leo,+ 28 na laana, ikiwa hamtatii amri za Yehova Mungu wenu+ na mkigeuka kutoka katika njia ninayowaamuru mfuate leo na mkifuata miungu mingine ambayo hamjaijua.

29 “Yehova Mungu wenu atakapowaleta katika nchi ambayo mtaimiliki, ni lazima mtangaze baraka kwenye Mlima Gerizimu na laana kwenye Mlima Ebali.+ 30 Je, haiko ng’ambo ya Yordani upande wa magharibi,* katika nchi ya Wakanaani wanaoishi Araba, mbele ya Gilgali, kando ya ile miti mikubwa ya More?+ 31 Kwa maana mnavuka Yordani mwingie na kuimiliki nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa ninyi.+ Mtakapoimiliki na kuishi humo, 32 ni lazima muwe waangalifu kutekeleza masharti na sheria zote ninazoweka* mbele yenu leo.+

12 “Haya ndiyo masharti na sheria ambazo mnapaswa kuwa waangalifu kutekeleza sikuzote mtakazokuwa hai katika nchi ambayo Yehova Mungu wa mababu zenu atawapa mwimiliki. 2 Mnapaswa kuharibu sehemu zote ambazo watu wa mataifa mtakaomiliki nchi yao wamekuwa wakiabudia miungu yao,+ iwe ni juu ya milima mirefu au kwenye vilima au chini ya mti wowote wenye majani mengi. 3 Mnapaswa kubomoa madhabahu zao, kuvunjavunja nguzo zao takatifu,+ kuteketeza kwa moto miti yao mitakatifu,* na kukatakata sanamu za kuchongwa za miungu yao,+ na kuondoa kabisa majina ya miungu yao kutoka sehemu hizo.+

4 “Hampaswi kumwabudu Yehova Mungu wenu kwa njia hiyo.+ 5 Badala yake, mtafuteni Yehova Mungu wenu mahali popote atakapochagua kuweka jina lake na mahali atakapokaa miongoni mwa makabila yote, mwende mahali hapo.+ 6 Hapo ndipo mnapopaswa kupeleka dhabihu zenu za kuteketezwa,+ matoleo yenu, sehemu zenu za kumi,+ mchango kutoka mkononi mwenu,+ dhabihu zenu za nadhiri, matoleo yenu ya hiari,+ na wazaliwa wa kwanza wa ng’ombe na kondoo wenu.+ 7 Ni lazima ninyi na familia zenu mle hapo mbele za Yehova Mungu wenu+ na kushangilia katika kazi zenu zote,+ kwa sababu Yehova Mungu wenu amewabariki.

8 “Msifanye kama tunavyofanya hapa leo, kila mtu anafanya jambo analoona ni jema machoni pake mwenyewe,* 9 kwa sababu bado hamjafika mahali pa kupumzika+ na katika urithi ambao Yehova Mungu wenu atawapa. 10 Mtakapovuka Yordani+ na kuishi katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu atawapa ili mwimiliki, kwa hakika atawapumzisha kutokana na maadui wenu wote wanaowazunguka, nanyi mtakaa kwa usalama.+ 11 Mtaleta vitu vyote ninavyowaamuru mahali ambapo Yehova Mungu wenu atachagua jina lake likae hapo+—dhabihu zenu za kuteketezwa, matoleo yenu, sehemu zenu za kumi,+ mchango kutoka mkononi mwenu, na kila dhabihu ya nadhiri mnayoweka nadhiri kwa Yehova. 12 Mtashangilia mbele za Yehova Mungu wenu,+ ninyi na wana wenu, binti zenu, watumwa wenu wa kiume na wa kike, na Mlawi yeyote aliye ndani ya majiji* yenu, kwa sababu hana fungu wala urithi pamoja nanyi.+ 13 Jihadharini msitoe dhabihu za kuteketezwa mahali pengine popote mtakapoona.+ 14 Mnapaswa kutoa dhabihu zenu za kuteketezwa mahali tu ambapo Yehova atachagua katika mojawapo ya maeneo ya makabila yenu, na huko ndiko mtakapofanya yote ninayowaamuru ninyi.+

15 “Lakini wakati wowote mnapotamani nyama, mtamchinja mnyama na kula nyama yake+ kulingana na baraka ambayo Yehova Mungu wenu amewapa katika majiji* yenu yote. Mtu asiye safi na mtu aliye safi anaweza kula, kama mnavyokula swala au paa. 16 Lakini msile damu kamwe;+ mnapaswa kuimwaga ardhini kama maji.+ 17 Hamtaruhusiwa kula ndani ya majiji* yenu sehemu ya kumi ya nafaka yenu, divai yenu mpya, mafuta yenu, wazaliwa wa kwanza wa ng’ombe na kondoo wenu,+ dhabihu yoyote mnayoweka nadhiri, matoleo yenu ya hiari, au mchango kutoka mkononi mwenu. 18 Mnapaswa kula vitu hivyo mbele za Yehova Mungu wenu mahali ambapo Yehova Mungu wenu atachagua+—ninyi na wana wenu, mabinti wenu, watumishi wenu wa kiume na vijakazi wenu, na Mlawi yeyote aliye ndani ya majiji* yenu; nanyi mtashangilia mbele za Yehova Mungu wenu katika kazi zenu zote. 19 Jihadharini msimpuuze Mlawi+ yeyote sikuzote mtakazoishi katika nchi yenu.

20 “Yehova Mungu wenu atakapopanua eneo lenu,+ kama alivyowaahidi,+ nanyi mseme, ‘Nataka kula nyama,’ kwa sababu mnatamani* kula nyama, mnaweza kula nyama wakati wowote mnapotamani kuila.+ 21 Ikiwa mahali ambapo Yehova Mungu wenu atachagua kuweka jina lake+ ni mbali kutoka kwenu, basi mnapaswa kuwachinja baadhi ya ng’ombe wenu au kondoo wenu ambao Yehova amewapa, kama nilivyowaamuru, nanyi mnapaswa kuwala ndani ya majiji* yenu wakati wowote mnapotamani nyama. 22 Mnaweza kuwala kama mnavyokula swala na paa;+ mtu asiye safi na mtu aliye safi anaweza kuila. 23 Ila tu mwazimie kwa uthabiti kutokula damu,+ kwa sababu damu ndiyo uhai,* nanyi hampaswi kula uhai*+ pamoja na nyama. 24 Msiile. Mnapaswa kuimwaga ardhini kama maji.+ 25 Msiile, ili mambo yawaendee vyema ninyi na watoto wenu baada yenu, kwa sababu mnafanya lililo sawa machoni pa Yehova. 26 Mnapaswa kuleta tu vitu vitakatifu ambavyo ni vyenu na dhabihu zenu za nadhiri mnapokuja mahali ambapo Yehova atachagua. 27 Mtatoa mahali hapo dhabihu zenu za kuteketezwa, nyama na damu,+ juu ya madhabahu ya Yehova Mungu wenu, na damu ya dhabihu zenu inapaswa kumwagwa kando ya madhabahu+ ya Yehova Mungu wenu, lakini mnaweza kula nyama.

28 “Muwe waangalifu kutii maneno haya yote ninayowaamuru ninyi, ili mambo yawaendee vyema sikuzote ninyi pamoja na wana wenu baada yenu, kwa sababu mnafanya mambo mema na yaliyo sawa machoni pa Yehova Mungu wenu.

29 “Yehova Mungu wenu atakapoyaangamiza mataifa ambayo mtamiliki nchi yao,+ na mtakapokuwa mkiishi katika nchi yao, 30 jihadharini msinaswe baada ya mataifa hayo kuangamizwa kutoka mbele yenu. Msiulize hivi kuhusu miungu yao: ‘Mataifa haya yaliabuduje miungu yake? Mimi pia nitafanya vivyo hivyo.’+ 31 Msimfanyie hivyo Yehova Mungu wenu, kwa sababu mataifa hayo yanaifanyia miungu yao kila jambo linalochukiza ambalo Yehova anachukia, hata kuwateketeza motoni wana na mabinti wao kwa ajili ya miungu yao.+ 32 Mnapaswa kutenda kwa uangalifu kila neno ninalowaamuru.+ Msiongeze wala kupunguza jambo lolote katika maneno hayo.+

13 “Ikiwa nabii au mtu anayebashiri kupitia ndoto atatokea miongoni mwenu na kuwapa ishara au dalili ya ajabu, 2 kisha ishara au dalili hiyo aliyowaambia itimie wakati anaposema, ‘Acheni tuifuate miungu mingine, miungu msiyoijua, na acheni tuiabudu,’ 3 hampaswi kusikiliza maneno ya nabii huyo au mwotaji huyo wa ndoto,+ kwa sababu Yehova Mungu wenu anawajaribu+ ili ajue ikiwa mnampenda Yehova Mungu wenu kwa moyo wenu wote na kwa nafsi* yenu yote.+ 4 Mnapaswa kumfuata Yehova Mungu wenu, mnapaswa kumwogopa yeye, mnapaswa kushika amri zake, mnapaswa kuisikiliza sauti yake; yeye ndiye mnayepaswa kumtumikia, nanyi mnapaswa kushikamana naye kabisa.+ 5 Lakini nabii huyo au mwotaji huyo wa ndoto anapaswa kuuawa,+ kwa sababu aliwachochea mmwasi Yehova Mungu wenu—aliyewatoa nchini Misri na kuwakomboa kutoka katika nyumba ya utumwa—ili mtoke katika njia ambayo Yehova Mungu wenu amewaamuru mtembee. Nanyi lazima mwondoe kilicho kiovu kutoka miongoni mwenu.+

6 “Ikiwa ndugu yako, mwana wa mama yako, au mwana wako au binti yako au mke wako mpendwa au rafiki yako wa karibu sana* atajaribu kukushawishi kwa siri, akisema, ‘Twende tukaabudu miungu mingine,’+ miungu ambayo wewe wala mababu zako hamwijui, 7 kutoka miongoni mwa miungu ya mataifa yanayowazunguka, yaliyo karibu nanyi au mbali nanyi, kutoka mwisho mmoja wa nchi mpaka mwisho mwingine wa nchi, 8 usikubali ushawishi wake wala kumsikiliza,+ wala usimsikitikie wala kumhurumia wala kumlinda; 9 badala yake, ni lazima umuue.+ Mkono wako unapaswa kuwa wa kwanza kumuua, kisha mikono ya watu wote itafuata.+ 10 Nawe lazima umuue kwa kumpiga mawe,+ kwa sababu alijaribu kukugeuza umwache Yehova Mungu wako, aliyekutoa nchini Misri, kutoka katika nyumba ya utumwa. 11 Hivyo, Waisraeli wote watasikia na kuogopa, na kamwe hawatafanya tena jambo lolote baya kama hilo miongoni mwenu.+

12 “Ikiwa mtasikia ikisemwa hivi katika mojawapo ya majiji yenu ambayo Yehova Mungu wenu anawapa mkae humo: 13 ‘Watu wasiofaa kitu wametokea miongoni mwenu ili kuwapotosha wakaaji wa jiji lao, wakisema, “Twendeni tukaabudu miungu mingine,” miungu ambayo hamwijui,’ 14 mnapaswa kupeleleza jambo hilo, kufanya uchunguzi kamili na kuuliza kwa makini;+ na ikithibitishwa ni kweli kwamba jambo hilo lenye kuchukiza limefanywa miongoni mwenu, 15 ni lazima muwaangamize kwa upanga wakaaji wa jiji hilo.+ Mtawaangamiza+ kwa upanga watu wa jiji hilo pamoja na kila kitu kilichomo, kutia ndani mifugo yao. 16 Kisha mtakusanya nyara zote za jiji hilo katikati ya uwanja wa jiji na kuliteketeza jiji hilo kwa moto, na nyara hizo zitakuwa dhabihu nzima ya kuteketezwa kwa Yehova Mungu wenu. Nalo litabaki rundo la magofu milele. Halipaswi kamwe kujengwa tena. 17 Mikono yenu haipaswi kuchukua kitu chochote kinachopaswa kuharibiwa,*+ ili Yehova aache hasira yake kali na kuwaonyesha rehema na huruma na kuwafanya mwongezeke, kama alivyowaapia mababu zenu.+ 18 Kwa maana mnapaswa kumtii* Yehova Mungu wenu kwa kushika amri zake zote ambazo ninawaamuru leo, na hivyo kufanya yaliyo sawa machoni pa Yehova Mungu wenu.+

14 “Ninyi ni wana wa Yehova Mungu wenu. Msijikatekate+ wala kunyoa upara kwenye mapaji ya nyuso zenu* kwa ajili ya mtu aliyekufa.+ 2 Kwa maana ninyi ni watu watakatifu+ kwa Yehova Mungu wenu, na Yehova amewachagua ninyi muwe watu wake, mali yake ya pekee,* kutoka kati ya mataifa yote duniani.+

3 “Msile kitu chochote kinachochukiza.+ 4 Hawa ndio wanyama mnaoweza kula:+ ng’ombe, kondoo, mbuzi, 5 paa, swala, kulungu, mbuzi mwitu, mbawala, kondoo mwitu, na kondoo wa mlimani. 6 Mnaweza kumla mnyama yeyote mwenye kwato zilizopasuka na zilizogawanyika mara mbili na ambaye anacheua. 7 Lakini hampaswi kuwala wanyama wafuatao wanaocheua au wenye kwato zilizogawanyika: ngamia, sungura, na wibari, kwa sababu wanacheua lakini kwato zao hazijapasuka. Wao si safi kwenu.+ 8 Pia, msimle nguruwe kwa sababu ana kwato zilizopasuka lakini hacheui. Yeye si safi kwenu. Msile kamwe nyama yao wala kugusa mizoga yao.

9 “Kati ya viumbe wote wanaoishi ndani ya maji, mnaweza kula wafuatao: Mnaweza kumla kiumbe yeyote mwenye mapezi na magamba.+ 10 Lakini hampaswi kumla kiumbe yeyote ambaye hana mapezi na magamba. Yeye si safi kwenu.

11 “Mnaweza kumla ndege yeyote aliye safi. 12 Lakini hampaswi kuwala ndege wafuatao: tai, furukombe, tumbusi mweusi,*+ 13 mwewe mwekundu, mwewe mweusi, kila aina ya ndege mbua, 14 kila aina ya kunguru, 15 mbuni, bundi, shakwe, kila aina ya kipanga, 16 bundi mdogo, bundi mwenye masikio marefu, batamaji, 17 mwari, tumbusi, mnandi, 18 korongo, kila aina ya kulastara, hudihudi, na popo. 19 Pia, kila kiumbe* mwenye mabawa anayeishi katika makundi makubwa si safi kwenu. Hawapaswi kuliwa. 20 Mnaweza kumla kiumbe yeyote safi anayeruka.

21 “Msimle mnyama yeyote aliyepatikana amekufa.+ Mnaweza kumpa mkaaji mgeni aliye ndani ya majiji yenu,* naye anaweza kumla, au mnyama huyo anaweza kuuzwa kwa mgeni. Kwa maana ninyi ni watu watakatifu kwa Yehova Mungu wenu.

“Msimchemshe mwanambuzi katika maziwa ya mama yake.+

22 “Ni lazima mtoe sehemu ya kumi ya mazao ya shambani yanayotokana na mbegu zenu mwaka baada ya mwaka.+ 23 Mtakula sehemu ya kumi ya nafaka yenu, divai yenu mpya, mafuta yenu, na wazaliwa wa kwanza wa ng’ombe wenu na kondoo wenu mbele za Yehova Mungu wenu mahali ambapo atachagua jina lake likae hapo,+ ili mjifunze kumwogopa Yehova Mungu wenu sikuzote.+

24 “Lakini ikiwa safari ni ndefu sana kwenu na hivyo hamwezi kupeleka vitu hivyo mahali ambapo Yehova Mungu wenu amechagua jina lake likae hapo,+ kwa sababu ni mbali sana (kwa sababu Yehova Mungu wenu atawabariki), 25 basi mnaweza kubadilisha vitu hivyo kwa pesa, na mbebe pesa hizo mikononi mwenu na kwenda mahali ambapo Yehova Mungu wenu atachagua. 26 Kisha mnaweza kutumia pesa hizo kununua chochote mnachotamani, iwe ni ng’ombe, kondoo, mbuzi, divai na vinywaji vingine vyenye kileo, na kitu chochote mpendacho; nanyi mtakula huko mbele za Yehova Mungu wenu na kushangilia, ninyi na familia zenu.+ 27 Na msimpuuze Mlawi yeyote aliye ndani ya majiji yenu,+ kwa sababu hana fungu wala urithi pamoja nanyi.+

28 “Mwishoni mwa kila miaka mitatu mnapaswa kuleta sehemu yote ya kumi ya mazao yenu ya mwaka huo na kuyahifadhi ndani ya majiji yenu.+ 29 Kisha Mlawi, ambaye hana fungu wala urithi kati yenu, mkaaji mgeni, yatima, na mjane aliye ndani ya majiji yenu atakuja kula na kushiba,+ ili Yehova Mungu wenu awabariki katika mambo yote mnayofanya.+

15 “Mwishoni mwa kila miaka saba mnapaswa kufuta madeni.+ 2 Hivi ndivyo mtakavyoyafuta: Kila mtu aliyemkopesha jirani yake atafuta deni hilo. Hapaswi kudai malipo kutoka kwa jirani au ndugu yake, kwa maana yatatangazwa yamefutwa kwa agizo la Yehova.+ 3 Mnaweza kudai malipo kutoka kwa mgeni,+ lakini mnapaswa kufuta deni lolote la ndugu yenu. 4 Hata hivyo, hakuna yeyote kati yenu anayepaswa kuwa maskini, kwa sababu hakika Yehova atawabariki+ katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa mwimiliki kama urithi, 5 lakini ikiwa tu mtatii kabisa sauti ya Yehova Mungu wenu na kushika kwa uangalifu amri yote hii ninayowapa leo.+ 6 Kwa maana Yehova Mungu wenu atawabariki kama alivyowaahidi, nanyi mtayakopesha mataifa mengi, lakini ninyi hamtahitaji kukopa;+ nanyi mtatawala mataifa mengi, lakini hayatawatawala.+

7 “Ikiwa mmoja wa ndugu zenu atakuwa maskini miongoni mwenu katika mojawapo ya majiji yaliyo katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa, msiifanye mioyo yenu iwe migumu au kumfumbia mkono ndugu yenu maskini.+ 8 Kwa maana mnapaswa kumfumbulia mkono wenu kwa ukarimu+ na kufanya yote mwezayo kumkopesha* chochote anachohitaji au alichopungukiwa. 9 Jihadharini wazo hili ovu lisiingie mioyoni mwenu: ‘Mwaka wa saba, mwaka wa kufuta madeni, umekaribia,’+ na hivyo mkatae kumtendea kwa ukarimu ndugu yenu aliye maskini na kukosa kumpa chochote. Akimlilia Yehova kuwahusu ninyi, mtakuwa mmetenda dhambi.+ 10 Mnapaswa kumpa kwa ukarimu,+ nanyi hampaswi* kumpa huku mkinung’unika, kwa sababu hiyo Yehova Mungu wenu atabariki kila kazi na kila jambo mnalofanya.+ 11 Kwa maana sikuzote kutakuwa na maskini nchini.+ Ndiyo sababu ninawaamuru hivi: ‘Mnapaswa kumfumbulia mkono wenu kwa ukarimu ndugu yenu anayeteseka na maskini katika nchi yenu.’+

12 “Ikiwa uliuziwa ndugu yako, mwanamume au mwanamke Mwebrania, naye amekutumikia kwa miaka sita, basi katika mwaka wa saba unapaswa kumwachilia huru.+ 13 Na ikiwa utamwachilia huru, usimwache aende mikono mitupu. 14 Mpe kwa ukarimu kitu fulani kutoka katika mifugo yako, uwanja wako wa kupuria, na shinikizo lako la mafuta na divai. Unapaswa kumpa kama vile ambavyo Yehova Mungu wako amekubariki. 15 Kumbuka kwamba ulikuwa mtumwa katika nchi ya Misri na Yehova Mungu wako akakukomboa. Ndiyo sababu leo ninakuamuru ufanye hivyo.

16 “Lakini akikuambia, ‘Sitakuacha!’ kwa sababu anakupenda wewe na familia yako, kwa maana amefurahia kuwa pamoja nawe,+ 17 utachukua msumari na kutoboa sikio lake kwa msumari huo mpaka upenye mlangoni, naye atakuwa mtumwa wako daima. Utamfanyia kijakazi wako vivyo hivyo. 18 Usione vigumu kumwachilia huru, naye aondoke, kwa sababu thamani ya utumishi wake kwa miaka sita aliyokutumikia ni mara mbili ya thamani ya utumishi wa mfanyakazi aliyeajiriwa, na Yehova Mungu wako amekubariki katika kila jambo ambalo lilifanywa.

19 “Unapaswa kumtakasa kila mzaliwa wa kwanza wa kiume wa ng’ombe wako na kondoo wako kwa ajili ya Yehova Mungu wako.+ Usimtumie mzaliwa wa kwanza wa ng’ombe dume wako kufanya kazi yoyote wala usimkate manyoya mzaliwa wa kwanza wa kondoo wako. 20 Wewe na familia yako mnapaswa kumla mbele za Yehova Mungu wenu mwaka baada ya mwaka mahali ambapo Yehova Mungu wenu atachagua.+ 21 Lakini ikiwa ana kasoro, yaani, ni mlemavu, ni kipofu, au ana kasoro nyingine kubwa, usimtoe dhabihu kwa Yehova Mungu wako.+ 22 Mnapaswa kumla ndani ya majiji* yenu, mtu asiye safi na aliye safi watamla, kama mnavyokula swala au paa.+ 23 Lakini hampaswi kula damu yake;+ mtaimwaga ardhini kama maji.+

16 “Adhimisheni mwezi wa Abibu* na msherehekee Pasaka ya Yehova Mungu wenu,+ kwa sababu katika mwezi wa Abibu, Yehova Mungu wenu aliwatoa nchini Misri wakati wa usiku.+ 2 Nanyi mnapaswa kumtolea Yehova Mungu wenu dhabihu ya Pasaka+ kutoka katika kondoo wenu na ng’ombe wenu,+ mahali ambapo Yehova atachagua jina lake likae hapo.+ 3 Hampaswi kula kitu chochote chenye chachu pamoja na dhabihu hiyo;+ kwa siku saba mnapaswa kula mikate isiyo na chachu, mikate ya mateso, kwa sababu mlitoka haraka katika nchi ya Misri.+ Fanyeni hivyo sikuzote za maisha yenu ili mkumbuke siku mliyotoka katika nchi ya Misri.+ 4 Msipatikane na unga wowote uliokandwa wenye chachu katika nchi yenu yote kwa siku saba,+ wala nyama yoyote mtakayotoa dhabihu siku ya kwanza jioni haipaswi kubaki usiku kucha mpaka asubuhi.+ 5 Hamtaruhusiwa kutoa dhabihu ya Pasaka katika jiji lolote tu kati ya majiji ambayo Yehova anawapa ninyi. 6 Bali mtafanya hivyo mahali ambapo Yehova Mungu wenu atachagua jina lake likae hapo. Mnapaswa kutoa dhabihu ya Pasaka wakati wa jioni mara tu baada ya jua kutua,+ wakati uleule mliotoka Misri. 7 Mtaipika na kuila+ mahali ambapo Yehova Mungu wenu atachagua,+ na asubuhi mtarudi kwenye mahema yenu. 8 Kwa siku sita mtakula mikate isiyo na chachu, na siku ya saba kutakuwa na kusanyiko takatifu kwa Yehova Mungu wenu. Hampaswi kufanya kazi yoyote.+

9 “Mtahesabu majuma saba. Mnapaswa kuanza kuhesabu majuma saba wakati mnapoanza kuvuna kwa mundu nafaka iliyo shambani.+ 10 Kisha mtafanya Sherehe ya Majuma kwa Yehova Mungu wenu+ kwa toleo la hiari linalotoka mkononi mwenu, kulingana na baraka ambazo Yehova Mungu wenu amewapa.+ 11 Nanyi mnapaswa kushangilia mbele za Yehova Mungu wenu, ninyi na wana wenu, mabinti wenu, watumwa wenu wa kiume, vijakazi wenu, Walawi walio ndani ya majiji* yenu, wakaaji wageni, mayatima, na wajane walio kati yenu, mahali ambapo Yehova Mungu wenu atachagua jina lake likae.+ 12 Kumbukeni kwamba mlikuwa watumwa Misri,+ nanyi mshike na kutekeleza masharti haya.

13 “Mnapaswa kufanya Sherehe ya Vibanda*+ kwa siku saba mnapokusanya nafaka kutoka katika uwanja wenu wa kupuria na kutoka katika shinikizo lenu la mafuta na divai. 14 Shangilieni wakati wa sherehe yenu,+ ninyi na wana wenu, mabinti wenu, watumwa wenu wa kiume, vijakazi wenu, Walawi, wakaaji wageni, mayatima, na wajane walio ndani ya majiji yenu. 15 Kwa siku saba mtamfanyia Yehova Mungu wenu sherehe+ mahali ambapo Yehova atachagua, kwa kuwa Yehova Mungu wenu atabariki mazao yenu yote na kila jambo mnalofanya,+ nanyi mtakuwa na shangwe kwelikweli.+

16 “Mara tatu kwa mwaka, wanaume wenu wote wanapaswa kwenda mbele za Yehova Mungu wenu mahali atakapochagua: katika Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu,+ Sherehe ya Majuma,+ na Sherehe ya Vibanda,*+ na hakuna yeyote kati yao anayepaswa kwenda mbele za Yehova mikono mitupu. 17 Zawadi ambayo kila mtu ataleta inapaswa kulingana na baraka ambazo Yehova Mungu wenu amempa.+

18 “Mnapaswa kuwaweka waamuzi+ na maofisa kwa ajili ya kila kabila katika majiji yenu yote ambayo Yehova Mungu wenu anawapa, nao lazima wawahukumu watu kwa hukumu ya uadilifu. 19 Msipotoshe haki,+ msipendelee,+ wala kukubali rushwa, kwa maana rushwa hupofusha macho ya wenye hekima+ na hupotosha maneno ya waadilifu. 20 Haki—mnapaswa kufuatia haki,+ ili mwendelee kuishi na kumiliki nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa ninyi.

21 “Msipande mti wa aina yoyote na kuufanya kuwa mti mtakatifu*+ karibu na madhabahu ya Yehova Mungu wenu ambayo mtajitengenezea.

22 “Wala hampaswi kujisimamishia nguzo takatifu,+ kitu ambacho Yehova Mungu wenu anachukia.

17 “Usimtolee Yehova Mungu wako dhabihu ya ng’ombe dume au kondoo mwenye kasoro au mwenye tatizo lolote, kwa sababu jambo hilo litakuwa chukizo kwa Yehova Mungu wako.+

2 “Ikiwa mwanamume au mwanamke atapatikana miongoni mwenu, katika mojawapo ya majiji ambayo Yehova Mungu wenu anawapa, aliye na mazoea ya kufanya uovu machoni pa Yehova Mungu wenu na kuvunja agano lake,+ 3 naye anapotoka na kuabudu miungu mingine na kuiinamia miungu hiyo au jua au mwezi au jeshi lote la mbinguni,+ jambo ambalo sijaamuru,+ 4 ukiambiwa au kusikia habari hiyo, unapaswa kuchunguza jambo hilo kikamili. Ikithibitishwa ni kweli+ kwamba jambo hilo lenye kuchukiza limefanywa katika Israeli, 5 utamtoa nje ya malango ya jiji lenu mwanamume au mwanamke ambaye amefanya uovu huo, na lazima mwanamume au mwanamke huyo auawe kwa kupigwa mawe.+ 6 Kwa ushahidi wa* mashahidi wawili au watatu+ yule anayepaswa kufa atauawa. Hapaswi kuuawa kwa ushahidi wa shahidi mmoja.+ 7 Mikono ya mashahidi inapaswa kuwa ya kwanza kumuua, kisha mikono ya watu wengine wote. Ni lazima mwondoe uovu miongoni mwenu.+

8 “Ikiwa kesi ambayo ni ngumu sana kwenu kuamua inatokea katika mojawapo ya majiji yenu, iwe ni kesi ya kuua*+ au dai la kisheria limezushwa, au tendo la ukatili limefanywa, au mizozo mingine, mnapaswa kwenda mahali ambapo Yehova Mungu wenu atachagua.+ 9 Nendeni kwa makuhani Walawi na kwa mwamuzi+ anayehudumu wakati huo, muwapelekee mashtaka yenu, nao watafanya uamuzi.+ 10 Kisha mnapaswa kutenda kulingana na uamuzi watakaofanya mahali hapo palipochaguliwa na Yehova. Muwe waangalifu kufanya mambo yote wanayowaagiza. 11 Mnapaswa kutenda kulingana na sheria watakayowaonyesha na kulingana na uamuzi watakaowatangazia.+ Msigeuke na kuacha uamuzi watakaofanya, na kwenda kulia au kushoto.+ 12 Mtu anayetenda kwa kimbelembele kwa kukataa kumsikiliza kuhani anayemhudumia Yehova Mungu wenu au kukataa kumsikiliza mwamuzi ni lazima afe.+ Ni lazima mwondoe uovu katika Israeli.+ 13 Basi watu wote watasikia na kuogopa, nao hawatatenda tena kwa kimbelembele.+

14 “Mtakapoingia katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa, mkaimiliki na kuishi humo, nanyi mseme, ‘Na tumweke mfalme juu yetu kama mataifa yote yanayotuzunguka,’+ 15 mnapaswa kumweka mfalme ambaye Yehova Mungu wenu atamchagua.+ Mnapaswa kumchagua mfalme kutoka miongoni mwa ndugu zenu. Hamruhusiwi kumweka mfalme ambaye ni mgeni, ambaye si ndugu yenu. 16 Hata hivyo, hapaswi kujipatia farasi wengi+ au kuwafanya watu warudi Misri kuchukua farasi wengi zaidi,+ kwa kuwa Yehova aliwaambia hivi: ‘Msirudi huko tena kamwe kupitia njia hii.’ 17 Wala hapaswi kuwa na wake wengi, ili moyo wake usipotoke;+ wala hapaswi kujipatia fedha na dhahabu nyingi sana.+ 18 Atakapoketi kwenye kiti cha ufalme wake, ni lazima ajiandikie kwenye kitabu* nakala ya Sheria hii, kwa kutumia nakala inayowekwa na makuhani Walawi.+

19 “Anapaswa kubaki nacho, naye lazima akisome sikuzote za maisha yake,+ ili ajifunze kumwogopa Yehova Mungu wake na kushika maneno yote ya Sheria hii na masharti haya kwa kuyatekeleza.+ 20 Hivyo moyo wake hautajikweza juu ya ndugu zake, naye hataacha amri hiyo na kwenda kulia au kushoto, ili aendelee kutawala kwa muda mrefu katika ufalme wake, yeye na wanawe katika Israeli.

18 “Makuhani Walawi, naam, kabila lote la Lawi, halitakuwa na fungu au urithi pamoja na Waisraeli. Watakula dhabihu zinazochomwa kwa moto zinazotolewa kwa Yehova, ambazo ni urithi wake.+ 2 Kwa hiyo hawapaswi kuwa na urithi kati ya ndugu zao. Yehova ndiye urithi wao, kama alivyowaambia.

3 “Sasa hii ndiyo haki ambayo makuhani wanastahili kutoka kwa watu: Mtu yeyote anayetoa dhabihu, iwe ni ng’ombe dume au kondoo anapaswa kumpa kuhani mguu wa mbele, mataya, na tumbo. 4 Mnapaswa kumpa mazao ya kwanza ya nafaka yenu, divai yenu mpya, mafuta yenu, na manyoya ya kwanza yaliyokatwa ya kondoo wenu.+ 5 Yehova Mungu wenu amewachagua wao pamoja na wana wao kutoka kati ya makabila yenu yote ili wahudumu katika jina la Yehova daima.+

6 “Lakini ikiwa Mlawi ataondoka katika mojawapo ya majiji yenu katika Israeli alimokuwa akiishi,+ naye angependa kwenda mahali ambapo Yehova anachagua,*+ 7 anaweza kuhudumu huko katika jina la Yehova Mungu wake kama wanavyofanya ndugu zake wote, Walawi, wanaosimama huko mbele za Yehova.+ 8 Atapokea kiasi kilekile cha chakula pamoja nao,+ mbali na malipo anayopata baada ya kuuza mali za mababu zake.

9 “Mtakapoingia katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa, msijifunze kuiga mazoea yenye kuchukiza ya mataifa hayo.+ 10 Asipatikane miongoni mwenu mtu yeyote anayemteketeza* motoni+ mwanawe au binti yake, mtu yeyote anayefanya uaguzi,*+ mtu yeyote anayefanya uchawi,+ mtu yeyote anayetafuta ishara za ubashiri,+ mlozi,+ 11 mtu yeyote anayewafunga wenzake kwa uchawi, mtu yeyote anayetafuta ushauri kutoka kwa watu wanaowasiliana na roho,+ mpiga ramli,+ au mtu yeyote anayetafuta habari kuhusu wafu.+ 12 Kwa maana mtu yeyote anayefanya mambo haya ni chukizo kwa Yehova, na kwa sababu ya mazoea haya yanayochukiza, Yehova Mungu wenu anayafukuza mataifa hayo kutoka mbele yenu. 13 Mnapaswa kudhihirisha kwamba hamna lawama mbele za Yehova Mungu wenu.+

14 “Kwa maana mataifa haya mnayomiliki nchi yao yalikuwa yakiwasikiliza wale waliozoea uchawi+ na uaguzi,*+ lakini Yehova Mungu wenu hajawaruhusu mfanye jambo lolote kama hilo. 15 Yehova Mungu wenu atawainulia nabii kama mimi kutoka kati ya ndugu zenu. Ni lazima mumsikilize.+ 16 Kwa sababu hilo ndilo mlilomwomba Yehova Mungu wenu kule Horebu katika siku ya kusanyiko,*+ mliposema, ‘Usiache tusikie sauti ya Yehova Mungu wetu au kuona tena moto huu mkubwa, tusije tukafa.’+ 17 Kisha Yehova akaniambia, ‘Jambo walilosema ni sawa. 18 Nitawainulia nabii+ kama wewe kutoka kati ya ndugu zao, nami nitaweka maneno yangu katika kinywa chake,+ naye atawaambia mambo yote nitakayomwamuru.+ 19 Naam, nitamwadhibu kila mtu ambaye hatasikiliza maneno yangu ambayo nabii huyo atasema katika jina langu.+

20 “‘Ikiwa nabii yeyote atasema kwa kimbelembele katika jina langu neno ambalo sikumwamuru aseme au kusema katika jina la miungu mingine, nabii huyo lazima afe.+ 21 Lakini huenda mkasema hivi mioyoni mwenu: “Tutajuaje Yehova hajasema neno hilo?” 22 Nabii akisema neno katika jina la Yehova na neno hilo lisitimie au kufanyika, basi Yehova hakusema neno hilo. Nabii huyo alilisema kwa kimbelembele. Hampaswi kumwogopa.’

19 “Yehova Mungu wenu atakapoyaangamiza mataifa ambayo Yehova Mungu wenu anawapa nchi yao na mtakapokuwa mmemiliki nchi yao na kuishi katika majiji yao na nyumba zao,+ 2 mnapaswa kutenga majiji matatu katikati ya nchi yenu ambayo Yehova Mungu wenu anawapa mwimiliki.+ 3 Mnapaswa kugawanya mara tatu eneo la nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa mwimiliki, nanyi mtengeneze barabara ili muuaji yeyote aweze kukimbilia katika mojawapo ya majiji hayo.

4 “Sasa hivi ndivyo itakavyokuwa kuhusu muuaji ambaye huenda akakimbilia humo ili kuokoa uhai wake: Akimuua jirani yake bila kukusudia naye hakuwa akimchukia;+ 5 kwa mfano, anapoenda na jirani yake msituni kukusanya kuni, kisha anainua mkono wake ili akate mti kwa shoka, lakini shoka lichomoke kwenye mpini na kumgonga jirani yake na kumuua, muuaji huyo anapaswa kukimbilia katika mojawapo ya majiji hayo.+ 6 Asipofanya hivyo, mtu anayelipiza kisasi cha damu+ anaweza kwa hasira kali kumkimbiza, kumkamata, na kumuua, kwa sababu jiji hilo lilikuwa mbali sana. Hata hivyo, hakustahili kufa kwa sababu hakuwa akimchukia jirani yake.+ 7 Ndiyo sababu ninawaamuru hivi: ‘Tengeni majiji matatu.’

8 “Yehova Mungu wenu akipanua eneo lenu kama alivyowaapia mababu zenu+ na kuwapa nchi yote aliyoahidi kuwapa mababu zenu+ 9 —maadamu mnashika kwa uaminifu amri hii yote ninayowapa leo, kwa kumpenda Yehova Mungu wenu na kutembea daima katika njia zake+—basi mtaongeza majiji mengine matatu zaidi ya hayo matatu.+ 10 Hivyo hakuna damu isiyo na hatia itakayomwagwa+ katika nchi yenu ambayo Yehova Mungu wenu anawapa kuwa urithi, nanyi hamtakuwa na hatia yoyote ya damu.+

11 “Lakini ikiwa mtu alikuwa akimchukia jirani yake,+ akamvizia, akamjeruhi vibaya sana na kumuua, na mtu huyo amekimbilia katika mojawapo ya majiji hayo, 12 basi wazee wa jiji lake wanapaswa kumwita kutoka humo na kumtia mikononi mwa yule anayelipiza kisasi cha damu, naye lazima afe.+ 13 Hampaswi kumhurumia,* nanyi lazima mwondoe hatia ya damu isiyo na hatia kutoka katika Israeli,+ ili mambo yawaendee vyema.

14 “Mtakapopokea urithi wenu katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa mwimiliki, hampaswi kusogeza alama ya mpaka+ wa jirani yenu kutoka mahali ambapo uliwekwa na mababu zenu.

15 “Shahidi mmoja hawezi kufanya mtu mwingine ahukumiwe kwa kosa lolote au dhambi yoyote ambayo huenda ametenda.+ Jambo hilo linapaswa kuthibitishwa kwa ushahidi wa* mashahidi wawili au mashahidi watatu.+ 16 Shahidi mwenye nia ya kumdhuru mwingine akitoa ushahidi dhidi ya mtu na kumshtaki kwa kosa fulani,+ 17 watu hao wawili wanaozozana watasimama mbele za Yehova, mbele ya makuhani na waamuzi watakaokuwa wakihudumu wakati huo.+ 18 Waamuzi watachunguza jambo hilo kikamili,+ na ikiwa mtu huyo ni shahidi wa uwongo na ameleta shtaka la uwongo dhidi ya ndugu yake, 19 mnapaswa kumtendea kama alivyopanga kumtendea ndugu yake kwa hila,+ nanyi lazima mwondoe uovu miongoni mwenu.+ 20 Wale wanaobaki watasikia na kuogopa, nao hawatatenda tena kamwe uovu kama huo miongoni mwenu.+ 21 Hampaswi* kuwahurumia:+ Uhai utatolewa kwa uhai,* jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono, mguu kwa mguu.+

20 “Mkienda vitani kupigana na maadui wenu na kuona kwamba farasi wao na magari yao ya vita na wanajeshi wao ni wengi kuliko ninyi, msiwaogope, kwa maana Yehova Mungu wenu aliyewatoa nchini Misri yuko pamoja nanyi.+ 2 Mnapokaribia kwenda vitani, kuhani anapaswa kuja na kuwahutubia watu.+ 3 Anapaswa kuwaambia hivi: ‘Sikilizeni, enyi Waisraeli, hivi punde mtapigana na maadui wenu. Msife moyo. Msiogope wala msihofu wala kutetemeka kwa sababu yao, 4 kwa maana Yehova Mungu wenu anapiga mwendo pamoja nanyi ili awapiganie dhidi ya maadui wenu na kuwaokoa ninyi.’+

5 “Maofisa pia wanapaswa kuwaambia watu hivi: ‘Ni nani ambaye amejenga nyumba mpya lakini hajaizindua? Na arudi nyumbani kwake. La sivyo, huenda akauawa vitani na mwanamume mwingine aizindue. 6 Na ni nani ambaye amepanda shamba la mizabibu na hajaanza kuvuna matunda yake? Na arudi nyumbani kwake. La sivyo, huenda akauawa vitani na mwanamume mwingine akaanza kuvuna matunda yake. 7 Na ni nani ambaye amemchumbia mwanamke lakini hajamwoa? Na arudi nyumbani kwake.+ La sivyo, huenda akauawa vitani na mwanamume mwingine amwoe.’ 8 Maofisa hao wanapaswa pia kuwauliza watu, ‘Ni nani anayeogopa na aliye na moyo dhaifu?+ Anapaswa kurudi nyumbani kwake, ili asiwafanye ndugu zake wavunjike moyo kama yeye.’*+ 9 Baada ya maofisa hao kuzungumza na watu, wanapaswa kuwaweka wakuu wa majeshi ili wawaongoze watu.

10 “Mnapokaribia jiji ili kupigana nalo, mnapaswa kulitangazia pia masharti ya amani.+ 11 Jiji hilo likikubali kufanya amani pamoja nanyi na kuwafungulia malango yake, watu wote waliomo humo watakuwa wafanyakazi wenu wa kazi za kulazimishwa, nao watawatumikia.+ 12 Lakini likikataa kufanya amani pamoja nanyi na kupigana nanyi, mnapaswa kulizingira, 13 na kwa hakika Yehova Mungu wenu atalitia mikononi mwenu, nanyi mtamuua kwa upanga kila mwanamume aliye ndani ya jiji hilo. 14 Hata hivyo, mtajichukulia wanawake, watoto, mifugo, na kila kitu kilicho jijini, nyara zake zote,+ nanyi mtakula nyara za maadui wenu ambazo Yehova Mungu wenu amewapa ninyi.+

15 “Hivyo ndivyo mtakavyoyatendea majiji yote yaliyo mbali sana nanyi ambayo si majiji ya mataifa haya yaliyo karibu. 16 Lakini katika majiji ya mataifa haya, ambayo Yehova Mungu wenu anawapa yawe urithi wenu, hampaswi kuacha hai kitu chochote kinachopumua.+ 17 Mnapaswa kuwaangamiza kabisa, Wahiti, Waamori, Wakanaani, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi,+ kama Yehova Mungu wenu alivyowaamuru; 18 ili wasiwafundishe kufuata mazoea yao yote yenye kuchukiza wanayofanyia miungu yao, na hivyo kuwafanya mumtendee dhambi Yehova Mungu wenu.+

19 “Mkilizingira jiji na kuliteka baada ya kupigana nalo kwa siku nyingi, hampaswi kuharibu miti yake kwa kuikata ovyoovyo kwa shoka. Mnaweza kula matunda yake, lakini hampaswi kuikata.+ Je, mnapaswa kuushambulia mti kama mnavyomshambulia mwanadamu? 20 Mnaweza kuharibu tu mti ambao mnajua hautumiwi kwa chakula. Mnaweza kuukata na kuutumia kulizingira jiji linalopigana nanyi, mpaka litakapoanguka.

21 “Mtu akipatikana ameuawa uwanjani katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa mwimiliki na haijulikani ni nani aliyemuua, 2 wazee na waamuzi+ wenu wanapaswa kwenda na kupima umbali kutoka kwenye maiti hiyo mpaka kwenye majiji yaliyo karibu nayo. 3 Kisha wazee wa jiji lililo karibu na maiti hiyo wanapaswa kuchukua kutoka kati ya mifugo ng’ombe mchanga ambaye hajawahi kutumiwa kufanya kazi, ambaye hajawahi kuvuta nira, 4 na wazee wa jiji hilo watampeleka ng’ombe huyo mchanga kwenye bonde* linalotiririka maji ambalo halijalimwa wala kupandwa mbegu, nao wanapaswa kumvunja shingo ng’ombe huyo mchanga humo bondeni.+

5 “Nao makuhani, Walawi, watakuja kwa sababu Yehova Mungu wenu amewachagua wamhudumie,+ watangaze baraka katika jina la Yehova.+ Watatangaza jinsi kila mzozo unaohusisha ukatili unavyopaswa kusuluhishwa.+ 6 Kisha wazee wote wa jiji lililo karibu zaidi na maiti hiyo wanapaswa kunawa mikono yao+ juu ya ng’ombe huyo mchanga ambaye alivunjwa shingo bondeni, 7 nao wanapaswa kutangaza hivi: ‘Mikono yetu haikumwaga damu hii, wala macho yetu hayakuona ikimwagwa. 8 Usiwahesabie hatia hiyo watu wako Waisraeli, ambao uliwakomboa,+ Ee Yehova, nawe usiache hatia ya damu isiyo na lawama ibaki miongoni mwa watu wako Waisraeli.’+ Nao hawatakuwa na hatia hiyo ya damu. 9 Kwa njia hiyo mtaondoa hatia ya damu isiyo na lawama kutoka miongoni mwenu kwa kufanya yaliyo sawa machoni pa Yehova.

10 “Mkienda vitani kupigana na maadui wenu na Yehova Mungu wenu awasaidie kuwashinda, nanyi mwachukue mateka,+ 11 ukiona mwanamke mrembo miongoni mwa mateka hao na kuvutiwa naye, nawe utake kumchukua awe mke wako, 12 unaweza kumleta nyumbani mwako. Kisha atanyoa kichwa chake, atatunza kucha zake, 13 na kuvua nguo alizokuwa amevaa alipotekwa, naye ataishi nyumbani mwako. Atamlilia baba yake na mama yake kwa mwezi mzima,+ kisha unaweza kulala naye; utakuwa mume wake naye atakuwa mke wako. 14 Lakini ikiwa hupendezwi naye, unapaswa kumruhusu aende zake+ mahali popote anapotaka. Lakini huwezi kumuuza upate pesa au kumtesa, kwa kuwa umemwaibisha.

15 “Ikiwa mwanamume ana wake wawili, naye anampenda mmoja zaidi ya mwenzake* na wote wawili wamemzalia wana na mzaliwa wa kwanza ni wa mwanamke asiyependwa sana,+ 16 siku atakapowapa wanawe urithi wake, hataruhusiwa kumtendea mwana wa mwanamke anayependwa kana kwamba ndiye mzaliwa wake wa kwanza na kumpuuza mwana wa mwanamke asiyependwa sana, ambaye ndiye mzaliwa wa kwanza. 17 Anapaswa kumtambua mwana wa mwanamke asiyependwa sana kuwa mzaliwa wa kwanza kwa kumpa maradufu ya kila kitu alicho nacho, kwa sababu mwana huyo ndiye mwanzo wa nguvu zake za uzazi. Haki ya mzaliwa wa kwanza ni yake.+

18 “Ikiwa mtu ana mwana ambaye ni mkaidi na mwasi na hamtii baba yake au mama yake,+ nao wamejaribu kumrekebisha lakini anakataa kuwasikiliza,+ 19 baba yake na mama yake wanapaswa kumshika na kumpeleka kwa wazee kwenye lango la jiji lake 20 na kuwaambia hivi wazee wa jiji lake: ‘Huyu mwana wetu ni mkaidi na mwasi, anakataa kututii. Ni mlafi+ na mlevi.’+ 21 Basi watu wote wa jiji lake watamuua kwa kumpiga mawe. Kwa hiyo ni lazima mwondoe uovu miongoni mwenu, na Waisraeli wote watasikia na kuogopa.+

22 “Mtu akitenda dhambi inayostahili hukumu ya kifo, naye ameuawa,+ na mmemtundika mtini,+ 23 maiti yake isibaki mtini usiku kucha.+ Badala yake, mnapaswa kuhakikisha kwamba mnaizika siku hiyohiyo, kwa sababu mtu aliyetundikwa ni kitu kilicholaaniwa na Mungu,+ nanyi hampaswi kuichafua nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa iwe urithi wenu.+

22 “Ukimwona ng’ombe dume wa ndugu yako au kondoo wake akipotea njia, usimpuuze kimakusudi.+ Unapaswa kumrudisha kwa ndugu yako. 2 Lakini ikiwa huyo ndugu yako haishi karibu nawe au humjui, unapaswa kumpeleka mnyama huyo nyumbani kwako, naye atakaa nawe mpaka ndugu yako atakapokuja kumtafuta. Kisha utamrudishia mnyama huyo.+ 3 Unapaswa kufanya vivyo hivyo kuhusu punda wake, nguo zake, na kitu chochote utakachopata kilichopotezwa na ndugu yako. Hupaswi kukipuuza.

4 “Ukimwona punda wa ndugu yako au ng’ombe dume wake akianguka barabarani hupaswi kumpuuza kimakusudi. Unapaswa kumsaidia kumwinua mnyama huyo.+

5 “Mwanamke hapaswi kuvaa nguo za mwanamume, na mwanamume hapaswi kuvaa nguo za mwanamke. Kwa maana mtu yeyote anayefanya hivyo ni chukizo kwa Yehova Mungu wenu.

6 “Ukipata njiani kiota cha ndege chenye makinda au mayai, iwe mtini au kwenye ardhi, naye mama amefunika makinda au kuatamia mayai, usimchukue mama pamoja na makinda yake.+ 7 Hakikisha umemfukuza mama yao, lakini unaweza kuchukua makinda. Fanya hivyo ili mambo yakuendee vyema na uishi muda mrefu.

8 “Ukijenga nyumba mpya, ni lazima pia ujenge ukuta kuzunguka ukingo wa paa lako,+ ili mtu asianguke kutoka kwenye paa nawe uiletee familia yako hatia ya damu.

9 “Usipande aina mbili za mbegu katika shamba lako la mizabibu.+ La sivyo, mazao yote utakayopata kutokana na mbegu hizo na pia zabibu zitakuwa za mahali patakatifu.

10 “Usilime kwa ng’ombe dume na punda pamoja.+

11 “Usivae nguo zilizotengenezwa kwa kuchanganya sufu na kitani.+

12 “Unapaswa kutengeneza vishada kwenye pembe nne za nguo unazovaa.+

13 “Mwanamume akimchukua mke na kufanya ngono naye lakini baadaye amchukie* 14 na kudai kwamba ana mwenendo mbaya na kumharibia sifa kwa kusema, ‘Nilimchukua mwanamke huyu, lakini nilipofanya ngono naye sikupata uthibitisho wa kwamba yeye ni bikira,’ 15 baba na mama ya msichana huyo wanapaswa kuwapelekea wazee walio kwenye lango la jiji uthibitisho wa kwamba msichana huyo alikuwa bikira. 16 Baba ya msichana huyo atawaambia hivi wazee hao: ‘Nilimpa mwanamume huyu binti yangu awe mke wake, lakini anamchukia* 17 na anadai kwamba ana mwenendo mbaya kwa kusema, “Nimegundua kwamba binti yenu si bikira.” Sasa huu ndio uthibitisho wa ubikira wa binti yangu.’ Kisha watatandaza nguo hiyo mbele ya wazee wa jiji. 18 Wazee wa jiji+ watamchukua mwanamume huyo na kumtia nidhamu.+ 19 Watamtoza shekeli 100 za fedha na kumpa baba ya msichana huyo, kwa sababu mtu huyo alimharibia sifa bikira wa Israeli,+ naye ataendelea kuwa mke wake. Maadamu mwanamume huyo anaishi, hataruhusiwa kumtaliki msichana huyo.

20 “Hata hivyo, ikiwa madai hayo ni ya kweli na hakuna uthibitisho kwamba msichana huyo alikuwa bikira, 21 wanapaswa kumpeleka msichana huyo kwenye mlango wa nyumba ya baba yake, na wanaume wa jiji watamuua kwa kumpiga mawe, kwa sababu ametenda jambo la aibu+ katika Israeli kwa kufanya uasherati* katika nyumba ya baba yake.+ Kwa hiyo ni lazima mwondoe uovu miongoni mwenu.+

22 “Mwanamume akipatikana akifanya ngono na mke wa mwanamume mwingine, ni lazima wote wawili wauawe pamoja, mwanamume huyo pamoja na mwanamke aliyefanya naye ngono.+ Kwa hiyo ni lazima mwondoe uovu katika Israeli.

23 “Ikiwa bikira amechumbiwa na mwanamume, kisha mwanamume mwingine akutane naye jijini na kufanya naye ngono, 24 mnapaswa kuwaleta wote wawili kwenye lango la jiji na kuwaua kwa kuwapiga mawe, mtamuua msichana huyo kwa sababu hakupiga mayowe jijini na mwanamume huyo kwa sababu alimwaibisha mke wa mwanamume mwenzake.+ Kwa hiyo ni lazima mwondoe uovu miongoni mwenu.

25 “Hata hivyo, ikiwa mwanamume huyo alimkuta uwanjani msichana huyo aliyechumbiwa na kumkamata kwa nguvu na kufanya naye ngono, mwanamume huyo aliyelala naye atauawa peke yake, 26 lakini msimtendee lolote msichana huyo. Msichana huyo hajatenda dhambi inayostahili kifo. Kisa chake ni sawa na cha mtu anayemshambulia mwenzake na kumuua.+ 27 Kwa maana mwanamume huyo alimkuta uwanjani, na msichana huyo aliyechumbiwa akapiga mayowe, lakini hakukuwa na mtu wa kumwokoa.

28 “Mwanamume akikutana na bikira ambaye hajachumbiwa kisha amkamate kwa nguvu na kufanya naye ngono, nao wagunduliwe,+ 29 mwanamume aliyefanya ngono na msichana huyo anapaswa kumpa baba ya msichana huyo shekeli 50 za fedha, naye atakuwa mke wake.+ Kwa sababu mwanamume huyo alimwaibisha, hataruhusiwa kumtaliki msichana huyo maisha yake yote.

30 “Hakuna mwanamume anayepaswa kumwoa* mke wa baba yake, ili asimwaibishe baba yake.*+

23 “Mwanamume yeyote aliyehasiwa kwa kuminywa mapumbu au kwa kukatwa uume wake hapaswi kuja katika kutaniko la Yehova.+

2 “Hakuna mwanaharamu anayepaswa kuingia katika kutaniko la Yehova.+ Hata kufikia kizazi cha kumi, hakuna mzao wake yeyote anayepaswa kuja katika kutaniko la Yehova.

3 “Hakuna Mwamoni au Mmoabu anayepaswa kuja katika kutaniko la Yehova.+ Hata kufikia kizazi cha kumi, hakuna mzao wao yeyote anayepaswa kuja katika kutaniko la Yehova, 4 kwa sababu hawakuwasaidia kwa kuwapa chakula na maji mlipokuwa njiani kutoka Misri,+ na kwa sababu walimkodi Balaamu mwana wa Beori kutoka Pethori kule Mesopotamia ili awalaani ninyi.+ 5 Lakini Yehova Mungu wenu alikataa kumsikiliza Balaamu.+ Badala yake, Yehova Mungu wenu alibadili laana hiyo ikawa baraka kwenu,+ kwa sababu Yehova Mungu wenu aliwapenda.+ 6 Hampaswi kamwe kuhangaikia hali yao wala kuwasaidia kupata ufanisi siku zenu zote.+

7 “Msimchukie Mwedomu, kwa sababu yeye ni ndugu yenu.+

“Msimchukie Mmisri, kwa maana mlikuwa wakaaji wageni katika nchi yao.+ 8 Kizazi cha tatu cha watoto wao kinaweza kuja katika kutaniko la Yehova.

9 “Mnapopiga kambi ili kuwashambulia maadui wenu, mnapaswa kuepuka kitu chochote kibaya.*+ 10 Ikiwa mwanamume ni mchafu kwa sababu ametokwa na shahawa usiku,+ anapaswa kwenda nje ya kambi, asirudi kambini. 11 Ifikapo jioni, anapaswa kuoga kwa maji, kisha anaweza kurudi kambini jua linapotua.+ 12 Mahali pa faragha* panapaswa kutengwa nje ya kambi, na mnapaswa kwenda kujisaidia huko. 13 Kati ya vifaa vyenu mtakuwa na kijiti. Mnapochuchumaa nje, mnapaswa kukitumia kuchimba shimo na kisha kufunika kinyesi chenu. 14 Kwa maana Yehova Mungu wenu anatembea katika kambi yenu+ ili awakomboe na kuwatia maadui wenu mikononi mwenu, na lazima kambi yenu iwe takatifu,+ ili asione kitu chochote kichafu ndani yenu, naye ageuke na kuacha kutembea pamoja nanyi.

15 “Mtumwa akimkimbia bwana wake na kuja kwako usimrudishe kwa bwana wake. 16 Anaweza kukaa pamoja nawe mahali popote atakapochagua katika mojawapo ya majiji yenu, popote anapopenda. Usimtese.+

17 “Binti yeyote wa Israeli hapaswi kuwa kahaba wa hekaluni, + wala mwana yeyote wa Israeli hapaswi kuwa kahaba wa hekaluni.+ 18 Hampaswi kuleta mapato ya mwanamke kahaba au mapato* ya mwanamume kahaba* katika nyumba ya Yehova Mungu wenu ili kutimiza nadhiri, kwa sababu vyote viwili ni chukizo kwa Yehova Mungu wenu.

19 “Usimtoze riba ndugu yako,+ iwe ni riba ya mkopo wa pesa, chakula, au kitu chochote kinachoweza kutozwa riba. 20 Unaweza kumtoza riba mgeni,+ lakini usimtoze riba ndugu yako,+ ili Yehova Mungu wako akubariki katika kazi zote utakazofanya katika nchi mnayoenda kumiliki.+

21 “Ukiweka nadhiri kwa Yehova Mungu wako,+ usikawie kuitimiza.+ Kwa maana Yehova Mungu wako kwa hakika atakudai; la sivyo, utakuwa umetenda dhambi.+ 22 Lakini usipoweka nadhiri, hutakuwa na hatia ya dhambi.+ 23 Unapaswa kutimiza maneno ya kinywa chako,+ na ni lazima utekeleze nadhiri uliyoweka kwa kinywa chako mwenyewe kama toleo la hiari kwa Yehova Mungu wako.+

24 “Ukiingia katika shamba la mizabibu la jirani yako, unaweza kula zabibu za kutosha mpaka utosheke, lakini hupaswi kutia zabibu zozote katika chombo chako.+

25 “Ukiingia katika shamba la nafaka la jirani yako, unaweza kukwanyua kwa mkono wako masuke yaliyokomaa, lakini hupaswi kutumia mundu kukata nafaka ya jirani yako.+

24 “Mwanamume akimwoa mwanamke lakini hapendezwi naye kwa sababu ameona jambo fulani lisilofaa kwake, ni lazima amwandikie mwanamke huyo cheti cha talaka,+ ampe, na kumruhusu aondoke nyumbani mwake.+ 2 Akiondoka katika nyumba hiyo, anaweza kwenda kuolewa na mwanamume mwingine.+ 3 Mwanamume huyo wa pili akimchukia* na kumwandikia cheti cha talaka, kisha ampe na kumruhusu aondoke nyumbani mwake, au mwanamume huyo wa pili aliyemwoa akifa, 4 mume wake wa kwanza aliyemfukuza hataruhusiwa kumchukua tena awe mke wake baada ya mwanamke huyo kutiwa unajisi, kwa maana jambo hilo ni chukizo kwa Yehova. Hampaswi kuleta dhambi katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa kuwa urithi.

5 “Mwanamume aliyeoa karibuni hapaswi kutumikia jeshini wala kupewa majukumu mengine yoyote. Anapaswa kuwa huru kwa mwaka mmoja na kubaki nyumbani ili amfurahishe mke wake.+

6 “Hakuna mtu anayepaswa kuchukua jiwe la chini la kusagia au jiwe la juu kuwa dhamana kwa ajili ya mkopo,*+ kwa sababu kufanya hivyo ni sawa na kuchukua riziki ya* mtu kuwa dhamana.

7 “Ikiwa mtu atapatikana akiwa amemteka nyara ndugu yake Mwisraeli, naye amemtesa na kumuuza,+ mtekaji nyara huyo lazima auawe.+ Mnapaswa kuondoa uovu miongoni mwenu.+

8 “Ikiwa ugonjwa wa ukoma* umetokea na kuenea, muwe waangalifu sana kufanya mambo yote ambayo makuhani Walawi watawaagiza mfanye.+ Muwe waangalifu kufanya kama tu nilivyowaamuru. 9 Kumbukeni jinsi Yehova Mungu wenu alivyomtendea Miriamu mlipokuwa njiani kutoka Misri.+

10 “Ukimkopesha jirani yako kitu chochote,+ hupaswi kuingia nyumbani mwake ili kuchukua kitu anachotoa kuwa dhamana. 11 Unapaswa kusimama nje, na mtu huyo uliyemkopesha anapaswa kukuletea nje kitu anachotoa kuwa dhamana. 12 Na ikiwa mtu huyo ni maskini, hupaswi kulala na kitu alichokupa kuwa dhamana.+ 13 Unapaswa kufanya yote uwezayo kumrudishia kitu alichokupa kuwa dhamana baada tu ya jua kutua, naye atakuwa na vazi lake anapoenda kulala,+ na atakubariki; nawe utakuwa mwadilifu mbele za Yehova Mungu wako.

14 “Usimlaghai kibarua mwenye uhitaji na maskini, awe ni mmoja wa ndugu zako au ni mkaaji mgeni katika nchi yenu, ndani ya majiji* yenu.+ 15 Unapaswa kumpa mshahara wake siku hiyohiyo,+ kabla ya jua kutua, kwa sababu ana uhitaji na uhai wake unategemea* mshahara wake. Usipofanya hivyo, atamlilia Yehova, nawe utakuwa na hatia ya dhambi.+

16 “Akina baba hawapaswi kuuawa kwa sababu ya dhambi za wana wao, na wana hawapaswi kuuawa kwa sababu ya dhambi za baba zao.+ Mtu anapaswa kuuawa kwa sababu ya dhambi yake mwenyewe.+

17 “Usipotoshe hukumu ya mkaaji mgeni au ya yatima,+ nawe hupaswi kuchukua vazi la mjane kuwa dhamana ya mkopo.*+ 18 Kumbukeni kwamba mlikuwa watumwa nchini Misri, na Yehova Mungu wenu akawakomboa kutoka huko.+ Ndiyo sababu ninawaamuru mfanye hivyo.

19 “Unapovuna mavuno yako shambani na kusahau tita shambani, usirudi kulichukua. Linapaswa kuachwa kwa ajili ya mkaaji mgeni, yatima, na mjane,+ ili Yehova Mungu wako akubariki katika kila jambo unalofanya.+

20 “Unapoupiga mzeituni ili kuangusha zeituni, hupaswi kurudia kufanya hivyo kwenye matawi yake. Matunda yanayobaki utamwachia mkaaji mgeni, yatima, na mjane.+

21 “Unapokusanya zabibu katika shamba lako la mizabibu, hupaswi kurudi kukusanya zabibu zilizobaki. Unapaswa kumwachia mkaaji mgeni, yatima, na mjane. 22 Kumbukeni kwamba mlikuwa watumwa nchini Misri. Ndiyo sababu ninawaamuru mfanye hivyo.

25 “Watu wakizozana, wanaweza kwenda kuwaona waamuzi,+ nao wataamua kesi yao na kumtangaza mtu asiye na hatia kuwa mwadilifu na aliye na hatia kuwa mwovu.+ 2 Ikiwa mtu mwovu anastahili kupigwa viboko,+ mwamuzi atamwagiza alale chini kifudifudi, na mtu huyo atapigwa viboko mbele yake. Idadi ya viboko inapaswa kulingana na uovu aliotenda. 3 Anaweza kumpiga kufikia viboko 40,+ lakini asizidishe. Akiendelea kumpiga viboko zaidi, ndugu yenu ataaibika machoni penu.

4 “Hupaswi kumfunga kinywa ng’ombe dume anapopura nafaka.+

5 “Ikiwa ndugu wanaishi pamoja na mmoja wao afe bila mwana, mke wa yule aliyekufa hapaswi kuolewa na mwanamume mwingine nje ya ukoo huo. Ndugu ya mume wake anapaswa kwenda kwake, amchukue awe mke wake, na kufunga naye ndoa ya ndugu mkwe.+ 6 Mtoto wa kwanza atakayemzaa ataendeleza jina la ndugu yake aliyekufa,+ ili jina lake lisifutiliwe mbali kutoka Israeli.+

7 “Sasa ikiwa mwanamume huyo hataki kumwoa mjane wa ndugu yake, mjane huyo anapaswa kwenda kwa wazee kwenye lango la jiji na kuwaambia, ‘Ndugu ya mume wangu amekataa kuhifadhi jina la ndugu yake katika Israeli. Amekataa kufunga nami ndoa ya ndugu mkwe.’ 8 Ni lazima wazee wa jiji lake wamwite na kuzungumza naye. Ikiwa atasisitiza hivi: ‘Sitaki kumwoa,’ 9 basi mjane wa ndugu yake atamkaribia mbele ya wazee, atamvua mwanamume huyo kiatu,+ kisha amtemee mate usoni na kusema, ‘Hivyo ndivyo anavyopaswa kutendewa mwanamume ambaye hatajenga familia ya ndugu yake.’ 10 Kisha, jina la familia* yake katika Israeli litakuwa ‘Familia* ya mtu aliyevuliwa kiatu.’

11 “Wanaume wawili wakipigana na mke wa mmoja wao aingilie kati ili kumlinda mume wake asipigwe, naye aunyooshe mkono wake na kumkamata sehemu za siri mwanamume anayepigana na mume wake, 12 ni lazima mumkate mkono mwanamke huyo. Hampaswi* kumhurumia.

13 “Hupaswi kuwa na aina mbili za mawe ya mizani katika mfuko wako,+ jiwe kubwa na dogo. 14 Hupaswi kuwa na aina mbili za vyombo vya kupimia*+ nyumbani mwako, kikubwa na kidogo. 15 Unapaswa kuwa na mawe ya kupimia yaliyo sahihi na ya haki na kipimo kilicho sahihi na cha haki, ili uendelee kuishi kwa muda mrefu katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa.+ 16 Kwa maana kila mtu asiyetenda haki ambaye anafanya mambo hayo ni chukizo kwa Yehova Mungu wenu.+

17 “Kumbukeni yale ambayo Waamaleki waliwatendea mlipokuwa njiani kutoka Misri,+ 18 jinsi walivyokutana nanyi njiani na kuwashambulia wale wote waliokuwa wakijikokota nyuma mlipokuwa mmechoka na kuishiwa nguvu. Hawakumwogopa Mungu. 19 Yehova Mungu wenu atakapokuwa amewapumzisha kutokana na maadui wenu wote wanaowazunguka katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa kuwa urithi ili mwimiliki,+ mnapaswa kuwaangamiza kabisa Waamaleki ili wasikumbukwe tena chini ya mbingu.+ Msisahau jambo hilo.

26 “Mwishowe mtakapoingia katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa kuwa urithi wenu, nanyi mmeimiliki na mnaishi ndani yake, 2 mtachukua baadhi ya mavuno ya kwanza ya mazao* yote ya ardhi, mtakayokusanya katika nchi yenu ambayo Yehova Mungu wenu anawapa, na kuyatia katika kikapu na kwenda mahali ambapo Yehova Mungu wenu atachagua jina lake likae hapo.+ 3 Mtaenda kwa kuhani atakayekuwa akihudumu wakati huo na kumwambia, ‘Leo nimekuja kumjulisha Yehova Mungu wako kwamba nimeingia katika nchi ambayo Yehova aliwaapia mababu zetu kwamba atatupa sisi.’+

4 “Kisha kuhani atachukua kikapu hicho kutoka mkononi mwako na kukiweka mbele ya madhabahu ya Yehova Mungu wako. 5 Halafu utatangaza hivi mbele za Yehova Mungu wako: ‘Baba yangu alikuwa Mwaramu aliyekuwa akitangatanga,*+ akashuka kwenda Misri+ na kukaa huko akiwa mgeni, akiwa na watu wachache wa familia yake.+ Lakini huko akawa taifa kubwa, lenye nguvu na lenye watu wengi.+ 6 Na Wamisri wakatutesa na kutukandamiza na kututumikisha kikatili.+ 7 Basi tukaanza kumlilia Yehova, Mungu wa mababu zetu, naye Yehova akasikia sauti yetu na kutazama mateso yetu na taabu yetu na kukandamizwa kwetu.+ 8 Mwishowe Yehova akatutoa Misri kwa mkono wenye nguvu na mkono ulionyooshwa+ na kwa matendo yanayotisha na kwa ishara na miujiza.+ 9 Kisha akatuleta mahali hapa na kutupatia nchi hii, nchi inayotiririka maziwa na asali.+ 10 Sasa nimeleta mavuno ya kwanza ya mazao ya ardhi ambayo Yehova amenipa.’+

“Ni lazima ukiweke kikapu hicho mbele za Yehova Mungu wako na kuinama mbele za Yehova Mungu wako. 11 Kisha utashangilia kwa sababu ya vitu vyote vyema ambavyo Yehova Mungu wako amekupa wewe na nyumba yako, wewe na Mlawi na mkaaji mgeni aliye miongoni mwenu.+

12 “Baada ya kutoa sehemu yote ya kumi+ ya mazao yako katika mwaka wa tatu, mwaka wa sehemu ya kumi, utampa sehemu hiyo Mlawi, mkaaji mgeni, yatima, na mjane, nao watakula na kushiba katika majiji*+ yenu. 13 Kisha utasema hivi mbele za Yehova Mungu wako: ‘Nimeondoa sehemu takatifu kutoka katika nyumba yangu na kumpa Mlawi, mkaaji mgeni, yatima, na mjane,+ kama ulivyoniamuru. Sijavunja wala kupuuza amri zako. 14 Sikuila nikiomboleza wala kutoa kisehemu chochote nikiwa mchafu au kutoa kisehemu chochote kwa ajili ya wafu. Nimetii sauti ya Yehova Mungu wangu na kufanya mambo yote uliyoniamuru. 15 Sasa tazama chini kutoka katika makao yako matakatifu, mbinguni, na kuwabariki watu wako Waisraeli na nchi ambayo umetupatia,+ kama ulivyowaapia mababu zetu,+ nchi inayotiririka maziwa na asali.’+

16 “Siku ya leo Yehova Mungu wako anakuamuru utekeleze masharti haya na sheria hizi.* Ni lazima uzishike na kuzitekeleza kwa moyo wako wote+ na nafsi* yako yote. 17 Leo Yehova amewatangazia kwamba atakuwa Mungu wenu mnapotembea katika njia zake na kushika masharti yake,+ amri zake,+ na sheria zake,*+ na mnaposikiliza sauti yake. 18 Na leo mmemtangazia Yehova kwamba mtakuwa watu wake, mali yake ya pekee,*+ kama alivyowaahidi, na kwamba mtashika amri zake zote 19 na kwamba atawakweza juu ya mataifa mengine yote ambayo ameyatokeza,+ akiwapa sifa na umaarufu na utukufu mnapothibitisha kwamba ninyi ni taifa takatifu kwa Yehova Mungu wenu,+ kama alivyoahidi.”

27 Kisha Musa pamoja na wazee wa Israeli wakawaamuru watu hivi: “Shikeni kila amri ninayowapa leo. 2 Na siku mtakayovuka Yordani kuingia katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa, mtapanga mawe makubwa na kuyapaka chokaa.*+ 3 Kisha mwandike juu yake maneno yote ya Sheria hii mtakapokuwa mmevuka, ili muweze kuingia katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa, nchi inayotiririka maziwa na asali, kama Yehova Mungu wa mababu zenu alivyowaahidi.+ 4 Mtakapokuwa mmevuka Yordani, mnapaswa kupanga mawe hayo kwenye Mlima Ebali+ na kuyapaka chokaa,* kama ninavyowaamuru leo. 5 Pia mtamjengea Yehova Mungu wenu madhabahu huko, madhabahu ya mawe. Msitumie vifaa vya chuma kuijenga.+ 6 Mnapaswa kuijenga madhabahu ya Yehova Mungu wenu kwa mawe ambayo hayajachongwa na kumtolea Yehova Mungu wenu dhabihu za kuteketezwa juu yake. 7 Mtatoa dhabihu za ushirika+ na kuzila mahali hapo,+ nanyi mtashangilia mbele za Yehova Mungu wenu.+ 8 Andikeni waziwazi maneno yote ya Sheria hii juu ya mawe hayo.”+

9 Kisha Musa na makuhani Walawi wakawaambia hivi Waisraeli wote: “Nyamazeni, msikilize, enyi Waisraeli. Siku ya leo mmekuwa watu wa Yehova Mungu wenu.+ 10 Ni lazima msikilize sauti ya Yehova Mungu wenu na kutekeleza amri zake+ na masharti yake, ninayowaamuru leo.”

11 Siku hiyo Musa akawaamuru watu hivi: 12 “Makabila yafuatayo yatasimama kwenye Mlima Gerizimu+ ili kuwabariki watu mtakapokuwa mmevuka Yordani: Simeoni, Lawi, Yuda, Isakari, Yosefu, na Benjamini. 13 Na makabila yafuatayo yatasimama kwenye Mlima Ebali+ ili kutangaza laana: Rubeni, Gadi, Asheri, Zabuloni, Dani, na Naftali. 14 Na Walawi watamwambia hivi kila Mwisraeli kwa sauti kubwa:+

15 “‘Amelaaniwa mtu anayetengeneza sanamu ya kuchongwa+ au sanamu ya chuma,*+ kitu kinachomchukiza Yehova,+ kilichotengenezwa na mikono ya fundi,* na ambaye amekificha.’ (Na watu wote watasema, ‘Amina!’*)

16 “‘Amelaaniwa mtu anayemdharau baba yake au mama yake.’+ (Na watu wote watasema, ‘Amina!’)

17 “‘Amelaaniwa mtu anayesogeza alama ya mpaka wa jirani yake.’+ (Na watu wote watasema, ‘Amina!’)

18 “‘Amelaaniwa mtu anayemfanya kipofu apotee njia.’+ (Na watu wote watasema, ‘Amina!’)

19 “‘Amelaaniwa mtu anayepotosha haki+ ya mkaaji mgeni, yatima, au mjane.’+ (Na watu wote watasema, ‘Amina!’)

20 “‘Amelaaniwa mtu anayefanya ngono na mke wa baba yake, kwa sababu amemwaibisha baba yake.’*+ (Na watu wote watasema, ‘Amina!’)

21 “‘Amelaaniwa mtu anayefanya ngono na mnyama yeyote.’+ (Na watu wote watasema, ‘Amina!’)

22 “‘Amelaaniwa mtu anayefanya ngono na dada yake, binti ya baba yake au binti ya mama yake.’+ (Na watu wote watasema, ‘Amina!’)

23 “‘Amelaaniwa mtu anayefanya ngono na mama mkwe wake.’+ (Na watu wote watasema, ‘Amina!’)

24 “‘Amelaaniwa mtu anayemvizia na kumuua jirani yake.’+ (Na watu wote watasema, ‘Amina!’)

25 “‘Amelaaniwa mtu anayekubali rushwa ili amuue mtu asiye na hatia.’+ (Na watu wote watasema, ‘Amina!’)

26 “‘Amelaaniwa mtu ambaye hataunga mkono maneno haya ya Sheria kwa kuyatekeleza.’+ (Na watu wote watasema, ‘Amina!’)

28 “Nanyi kwa hakika mkiisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu kwa kuwa waangalifu kutenda amri zake zote ninazowaamuru leo, kwa hakika Yehova Mungu wenu atawakweza juu ya mataifa mengine yote ya dunia.+ 2 Baraka hizi zote zitawajia na kuwatangulia,+ kwa sababu mnaendelea kuisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu:

3 “Mtabarikiwa jijini na mtabarikiwa shambani.+

4 “Watoto wenu*+ watabarikiwa na pia mazao ya ardhi yenu na watoto wa mifugo yenu, ng’ombe wenu wachanga na wanakondoo wenu.+

5 “Kikapu chenu+ na bakuli lenu la kukandia litabarikiwa.+

6 “Mtabarikiwa mnapoingia ndani, na mtabarikiwa mnapotoka nje.

7 “Yehova atafanya maadui wanaowashambulia washindwe mbele yenu.+ Watawashambulia kutoka upande mmoja, lakini watawakimbia wakielekea pande saba tofauti.+ 8 Yehova atawaagizia baraka katika maghala yenu+ na katika kila kazi mnayofanya, na kwa hakika atawabariki katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa. 9 Yehova atawafanya kuwa taifa lake takatifu,+ kama alivyowaapia,+ kwa sababu mnaendelea kushika amri za Yehova Mungu wenu na kutembea katika njia zake. 10 Mataifa yote duniani yatalazimika kuona kwamba mmeitwa kwa jina la Yehova,+ nayo yatawaogopa ninyi.+

11 “Yehova atawafanya muwe na watoto wengi sana na mifugo mingi sana na mazao mengi sana+ katika nchi ambayo Yehova aliwaapia mababu zenu kwamba atawapa ninyi.+ 12 Yehova atawafungulia ghala lake zuri, mbingu, ili mvua inyeshe juu ya nchi yenu katika majira yake+ na kubariki kila jambo mnalofanya. Mtayakopesha mataifa mengi, lakini ninyi wenyewe hamtahitaji kukopa.+ 13 Yehova atawafanya kuwa kichwa wala si mkia; nanyi mtakuwa juu+ wala si chini, mkiendelea kutii amri za Yehova Mungu wenu ninazowaamuru leo mzishike na kuzitenda. 14 Msikengeuke kutoka katika maneno yote ninayowaamuru ninyi leo, na kwenda kulia au kushoto,+ kwa kufuata miungu mingine ili kuiabudu.+

15 “Lakini msipoisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu kwa kuwa waangalifu kutenda amri zake zote na sheria zake ninazowaamuru leo, laana hizi zote zitawajia na kuwatangulia:+

16 “Mtalaaniwa jijini na mtalaaniwa shambani.+

17 “Kikapu chenu+ na bakuli lenu la kukandia+ vitalaaniwa.

18 “Watoto wenu*+ na mazao ya ardhi yenu na ng’ombe wenu wachanga na wanakondoo wenu watalaaniwa.+

19 “Mtalaaniwa mnapoingia ndani na mtalaaniwa mnapotoka nje.

20 “Yehova atawaletea laana, vurugu na adhabu katika kila kazi mnayofanya mpaka mtakapoangamizwa na kutoweka upesi, kwa sababu ya mazoea yenu maovu na kuniacha mimi.+ 21 Yehova atafanya magonjwa yawaandame mpaka atakapokuwa amewaangamiza kutoka katika nchi mnayoenda kuimiliki.+ 22 Yehova atawapiga kwa kifua kikuu, homa kali,+ mwasho, joto la homa, upanga,+ upepo unaochoma, na kuvu;+ navyo vitawaandama mpaka mtakapoangamia. 23 Anga lililo juu ya vichwa vyenu litakuwa shaba, na dunia iliyo chini yenu itakuwa chuma.+ 24 Yehova atafanya mvua ya nchi yenu iwe ungaunga na mavumbi ambayo yatawanyeshea kutoka mbinguni mpaka mtakapoangamia kabisa. 25 Yehova atafanya mshindwe mbele ya maadui wenu.+ Mtawashambulia kutoka upande mmoja, lakini mtawakimbia mkielekea pande saba tofauti; nanyi mtakuwa kitu cha kutisha kwa falme zote za dunia.+ 26 Na maiti zenu zitakuwa chakula kwa kila ndege wa angani na mnyama wa ardhini, na hakuna mtu atakayewafukuza.+

27 “Yehova atawapiga kwa majipu ya Misri, bawasiri, ukurutu, na upele wa ngozi, nanyi hamtaweza kupona magonjwa hayo. 28 Yehova atawaletea kichaa na upofu+ na kuwafanya mchanganyikiwe.* 29 Mtapapasa-papasa wakati wa adhuhuri, kama kipofu anavyopapasa-papasa gizani,+ nanyi hamtafanikiwa katika jambo lolote mnalofanya; na watu watawalaghai na kuwanyang’anya vitu vyenu daima, na hakuna atakayewaokoa.+ 30 Utamchumbia mwanamke, lakini mwanamume mwingine atambaka. Utajenga nyumba, lakini hutaishi ndani yake.+ Utapanda shamba la mizabibu, lakini hutaanza kula matunda yake.+ 31 Ng’ombe dume wako atachinjwa mbele ya macho yako, lakini hutakula nyama yake. Punda wako ataibwa mbele ya macho yako, lakini hatarudishwa. Maadui wako watapewa kondoo wako, lakini hakuna atakayekusaidia. 32 Watu wengine watapewa wana wako na mabinti wako+ huku ukitazama, na sikuzote utatamani kuwaona, lakini mikono yako haitakuwa na nguvu za kufanya chochote. 33 Mavuno ya ardhi yako na mazao yako yote yataliwa na watu usiowajua,+ na sikuzote watu watawalaghai na kuwakandamiza. 34 Mtashikwa na kichaa kwa sababu ya mambo mtakayoona kwa macho yenu.

35 “Yehova atayapiga magoti yenu na miguu yenu kwa majipu yenye maumivu makali na yasiyopona, kuanzia nyayo za miguu yenu mpaka utosini. 36 Yehova atawapeleka ninyi na mfalme mliyemchagua awe juu yenu, kwenye taifa ambalo ninyi hamlijui wala mababu zenu hawakulijua,+ na huko mtaabudu miungu mingine, miungu ya miti na ya mawe.+ 37 Nanyi mtakuwa kitu cha kutisha na cha kudharauliwa,* na kitu cha kudhihakiwa miongoni mwa mataifa yote ambako Yehova atawapeleka.+

38 “Mtapanda mbegu nyingi shambani, lakini mtavuna mazao machache,+ kwa sababu nzige watayala.⁠ 39 Mtapanda na kupalilia mashamba ya mizabibu, lakini hamtakunywa divai kamwe wala kukusanya zabibu zozote,+ kwa sababu kiwavi atazila. 40 Mtakuwa na mizeituni katika eneo lenu lote, lakini hamtajipaka mafuta yoyote, kwa sababu zeituni zenu zitaanguka. 41 Mtazaa wana na mabinti, lakini hawataendelea kuwa wenu, kwa sababu watapelekwa utekwani.+ 42 Makundi ya wadudu* yatavamia miti yenu yote na mazao ya ardhi yenu. 43 Mkaaji mgeni aliye miongoni mwenu ataendelea kupanda juu yenu zaidi na zaidi, huku ninyi mkiendelea kushuka chini zaidi na zaidi. 44 Atawakopesha, lakini ninyi hamtamkopesha.+ Atakuwa kichwa, lakini ninyi mtakuwa mkia.+

45 “Laana hizi zote+ hakika zitawajia na kuwafuatia na kuwatangulia mpaka mtakapokuwa mmeangamizwa,+ kwa sababu hamkuisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu kwa kushika amri zake na sheria zake alizowaamuru.+ 46 Nazo zitaendelea kuwaandama ninyi na wazao wenu kama ishara na dalili ya kudumu,+ 47 kwa sababu hamkumtumikia Yehova Mungu wenu kwa furaha na shangwe moyoni mlipokuwa na wingi wa kila kitu.+ 48 Yehova atawatuma maadui wenu wawashambulie, nanyi mtawatumikia+ mkiwa na njaa+ na kiu na uchi na mkiwa maskini kabisa.* Ataweka nira ya chuma kwenye shingo zenu mpaka atakapokuwa amewaangamiza.

49 “Yehova ataleta dhidi yenu taifa la mbali,+ kutoka mwisho wa dunia; litawarukia kama tai,+ taifa ambalo hamtaelewa lugha yake,+ 50 taifa lenye uso mkali ambalo haliwajali wazee wala kuwahurumia vijana.+ 51 Watu hao watawala watoto wa mifugo yenu na mazao ya ardhi yenu mpaka mtakapokuwa mmeangamizwa. Hawatawaachia nafaka yoyote, divai mpya wala mafuta, ng’ombe mchanga wala mwanakondoo mpaka watakapokuwa wamewaangamiza.+ 52 Watawazingira na kuwafungia ndani ya majiji* yenu yote, katika nchi yenu yote, mpaka kuta zenu ndefu na zenye ngome mnazozitegemea zitakapoanguka. Naam, kwa hakika watawazingira katika majiji yenu yote, katika nchi yenu yote ambayo Yehova Mungu wenu amewapa ninyi.+ 53 Ndipo mtakapolazimika kuwala watoto wenu* wenyewe, nyama ya wana wenu na mabinti wenu+ ambao Yehova Mungu wenu amewapa, kwa sababu ya kuzingirwa kabisa na kwa sababu ya mateso yatakayosababishwa na adui yenu.

54 “Hata mwanamume mpole sana na aliyedekezwa miongoni mwenu hatamhurumia ndugu yake au mke wake mpendwa au wanawe wanaobaki, 55 naye hatawagawia hata kidogo nyama ya wanawe ambayo atakula, kwa sababu hana kitu kingine chochote cha kula kwa sababu ya kuzingirwa kabisa na kwa sababu ya mateso yatakayosababishwa na adui yenu katika majiji yenu.+ 56 Na mwanamke mpole sana na aliyedekezwa miongoni mwenu ambaye hata hawezi kuthubutu kukanyaga chini kwa wayo wa mguu wake kwa sababu ya kudekezwa sana+ hatamhurumia mume wake mpendwa wala mwanawe wala binti yake, 57 wala hata kondo la nyuma linalotoka katikati ya miguu yake wala wana anaozaa, kwa sababu atawala kwa siri kwa sababu ya kuzingirwa kabisa na kwa sababu ya mateso yatakayosababishwa na adui yenu katika majiji yenu.

58 “Ikiwa hamtashika kwa uangalifu maneno yote ya Sheria hii ambayo yameandikwa katika kitabu hiki+ na msipoliogopa jina hili tukufu na lenye kuogopesha,+ la Yehova+ Mungu wenu, 59 Yehova atawatesa ninyi na wazao wenu kwa mapigo makali sana, mapigo makubwa yanayodumu,+ na magonjwa hatari yanayodumu. 60 Atawaletea tena magonjwa yote ya Misri mliyokuwa mkiogopa, nayo kwa hakika yatawaandama ninyi. 61 Isitoshe, Yehova atawaletea pia kila ugonjwa au pigo ambalo halijaandikwa katika kitabu hiki cha Sheria mpaka mtakapoangamia. 62 Ingawa mmekuwa wengi sana kama nyota za mbinguni,+ ni wachache sana miongoni mwenu watakaobaki,+ kwa sababu hamkuisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu.

63 “Na kama Yehova alivyopendezwa wakati mmoja kuwafanikisha na kuwafanya mwongezeke, ndivyo Yehova atakavyopendezwa kuwaharibu na kuwaangamiza; nanyi mtang’olewa kutoka katika nchi mnayokaribia kuimiliki.

64 “Yehova atawatawanya miongoni mwa mataifa yote, kutoka mwisho mmoja wa dunia mpaka mwisho mwingine wa dunia,+ na huko mtalazimika kuabudu miungu ya miti na mawe, ambayo wala ninyi wala mababu zenu hamwijui.+ 65 Hamtakuwa na amani miongoni mwa mataifa hayo+ wala mahali pa kupumzisha wayo wa mguu wenu. Badala yake, mkiwa huko Yehova atawapa moyo wenye mahangaiko+ na macho yanayodhoofika na hisia za kukata tamaa.*+ 66 Uhai wenu utakabili hatari kubwa, nanyi mtaogopa usiku na mchana; nanyi hamtakuwa na uhakika wa kuokoka. 67 Asubuhi mtasema, ‘Laiti ingekuwa jioni!’ na jioni mtasema, ‘Laiti ingekuwa asubuhi!’ kwa sababu ya woga mtakaohisi mioyoni mwenu na kwa sababu ya mambo ambayo macho yenu yataona. 68 Na hakika Yehova atawarudisha Misri kwa meli, kupitia ile njia niliyowaambia hivi kuihusu: ‘Hamtaiona tena kamwe,’ na huko mtalazimika kujiuza kwa maadui wenu ili kuwa watumwa wa kiume na wa kike, lakini hakutakuwa na mtu wa kuwanunua.”

29 Haya ndiyo maneno ya agano ambalo Yehova alimwamuru Musa afanye pamoja na Waisraeli katika nchi ya Moabu, mbali na agano alilofanya nao kule Horebu.+

2 Kisha Musa akawaita Waisraeli wote na kuwaambia, “Mmeona mambo yote ambayo Yehova alifanya mbele ya macho yenu katika nchi ya Misri, mambo ambayo alimtendea Farao na watumishi wake wote na nchi yake yote,+ 3 hukumu kubwa ambazo* macho yenu yaliona, zile ishara kubwa na miujiza.+ 4 Lakini mpaka leo hii Yehova hajawapa moyo wa kuelewa na macho ya kuona na masikio ya kusikia.+ 5 ‘Nilipokuwa nikiwaongoza kwa miaka 40 nyikani,+ nguo mlizovaa hazikuchakaa na viatu mlivyovaa havikuchakaa miguuni mwenu.+ 6 Hamkula mkate wala kunywa divai wala kinywaji chochote chenye kileo, ili mjue kwamba mimi ni Yehova Mungu wenu.’ 7 Mwishowe mkafika mahali hapa, na Sihoni mfalme wa Heshboni+ na Ogu mfalme wa Bashani+ wakaja kupigana nasi, lakini tukawashinda.+ 8 Baada ya hayo tukachukua nchi yao na kuwapa Warubeni, Wagadi, na nusu ya kabila la Manase iwe urithi wao.+ 9 Kwa hiyo, shikeni maneno ya agano hili na kuyatii, ili kila jambo mnalofanya lifanikiwe.+

10 “Leo ninyi nyote mmesimama mbele za Yehova Mungu wenu; viongozi wa makabila yenu, wazee wenu, maofisa wenu, kila mwanamume wa Israeli, 11 watoto wenu, wake zenu,+ na mkaaji mgeni+ anayeishi kambini mwenu, kuanzia mtu anayewakusanyia kuni mpaka anayewatekea maji. 12 Mko hapa ili mwingie katika agano la Yehova Mungu wenu na kiapo chake, agano ambalo Yehova Mungu wenu anafanya pamoja nanyi leo+ 13 ili leo awafanye ninyi kuwa watu wake+ na ili awe Mungu wenu,+ kama alivyowaahidi ninyi na kama alivyowaapia mababu zenu, Abrahamu,+ Isaka,+ na Yakobo.+

14 “Sasa sifanyi agano hili na kiapo hiki pamoja nanyi tu, 15 bali nafanya pamoja na ninyi mnaosimama hapa pamoja nasi leo mbele za Yehova Mungu wetu na pamoja na wale ambao leo hawapo hapa pamoja nasi. 16 (Kwa maana ninyi mnajua vizuri jinsi tulivyoishi nchini Misri na jinsi tulivyopita katikati ya mataifa mbalimbali tulipokuwa safarini.+ 17 Nanyi mlikuwa mkiona vitu vyao vinavyochukiza na sanamu zao zenye kuchukiza*+ za miti na mawe, fedha na dhahabu, walizokuwa nazo.) 18 Jihadharini kusiwe na mwanamume au mwanamke, familia au kabila lolote kati yenu leo ambalo moyo wake utageuka na kumwacha Yehova Mungu wetu ili kwenda kuabudu miungu ya mataifa hayo,+ ili miongoni mwenu kusiwe na mzizi unaozaa tunda lenye sumu na pakanga.+

19 “Lakini mtu akisikia maneno ya kiapo hiki na kujigamba moyoni mwake akisema, ‘Nitakuwa na amani, ingawa ninasisitiza kwamba nitaendelea kutembea katika njia za moyo wangu mwenyewe,’ na hivyo kuharibu kila kitu* kilicho kwenye njia yake, 20 Yehova hatakuwa tayari kumsamehe.+ Badala yake, hasira kali ya Yehova itawaka dhidi ya mtu huyo, na laana yote iliyoandikwa katika kitabu hiki hakika itampata,+ na Yehova kwa kweli atafutilia mbali jina la mtu huyo kutoka duniani.* 21 Kisha Yehova atamtenga kutoka katika makabila yote ya Waisraeli ili apate msiba kulingana na laana yote ya agano iliyoandikwa katika kitabu hiki cha Sheria.

22 “Kizazi cha wakati ujao cha wana wenu na pia wageni kutoka nchi ya mbali watakapoona mapigo ya nchi, magonjwa ambayo Yehova ameleta juu yake— 23 kiberiti na chumvi na kuteketea, hivi kwamba nchi yote haitapandwa wala kuchipuza mimea, wala hakuna mmea wowote utakaoota ndani yake, kama ilivyokuwa wakati wa maangamizi ya Sodoma na Gomora,+ Adma na Seboiimu,+ majiji ambayo Yehova aliyaangamiza katika hasira yake na katika ghadhabu yake— 24 wao pamoja na mataifa yote watauliza, ‘Kwa nini Yehova aliitendea hivi nchi hii?+ Ni nini kilichomfanya awake hasira kali hivi?’ 25 Kisha watasema, ‘Ni kwa sababu waliliacha agano la Yehova,+ Mungu wa mababu zao, ambalo alifanya pamoja nao alipowatoa nchini Misri.+ 26 Lakini walienda na kuabudu miungu mingine na kuiinamia, miungu ambayo hawakuwa wameijua na ambayo hakuwaruhusu waiabudu.*+ 27 Ndipo hasira kali ya Yehova ikawaka dhidi ya nchi hiyo, naye akailetea nchi hiyo laana yote iliyoandikwa katika kitabu hiki.+ 28 Kwa hiyo, Yehova akawang’oa kutoka katika ardhi yao kwa hasira yake+ na ghadhabu kali na hamaki na kuwapeleka katika nchi nyingine, mahali walipo mpaka leo.’+

29 “Mambo yaliyofichwa ni ya Yehova Mungu wetu,+ lakini mambo yaliyofunuliwa ni yetu na wazao wetu milele, ili tutekeleze maneno yote ya Sheria hii.+

30 “Maneno haya yote yatakapotimia kwenu, baraka na laana ambayo nimeweka mbele yenu,+ nanyi myakumbuke*+ katika mataifa yote ambako Yehova Mungu wenu atawatawanya,+ 2 nanyi mrudi kwa Yehova Mungu wenu+ na kuisikiliza sauti yake kulingana na yote ninayowaamuru leo, ninyi na wana wenu, kwa moyo wenu wote na kwa nafsi* yenu yote,+ 3 ndipo Yehova Mungu wenu atakapowarudisha mateka wenu+ na kuwaonyesha ninyi rehema+ na kuwakusanya tena kutoka katika mataifa yote ambako Yehova Mungu wenu aliwatawanya.+ 4 Hata watu wenu wakitawanywa mpaka mwisho wa mbingu, Yehova Mungu wenu atawakusanya na kuwarudisha kutoka huko.+ 5 Yehova Mungu wenu atawarudisha katika nchi ambayo baba zenu walimiliki, nanyi mtaimiliki; naye atawafanikisha na kuwafanya mwongezeke kuliko baba zenu.+ 6 Yehova Mungu wenu ataisafisha* mioyo yenu na mioyo ya wazao wenu,+ ili mumpende Yehova Mungu wenu kwa moyo wenu wote na kwa nafsi* yenu yote na ili muweze kuishi.+ 7 Ndipo Yehova Mungu wenu atawaletea laana hizi zote maadui wenu, waliowachukia na kuwatesa.+

8 “Kisha mtarudi na kuisikiliza sauti ya Yehova na kushika amri zake zote ninazowaamuru leo. 9 Yehova Mungu wenu atawaletea mafanikio mengi katika kazi yote ya mikono yenu,+ atawafanya muwe na watoto wengi na mifugo mingi na mazao mengi ya ardhi yenu, kwa maana Yehova atafurahia tena kuwafanikisha, kama alivyofurahia kuwafanikisha mababu zenu.+ 10 Kwa maana wakati huo mtaisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu na kushika amri zake na sheria zilizoandikwa katika kitabu hiki cha Sheria, nanyi mtarudi kwa Yehova Mungu wenu kwa moyo wenu wote na kwa nafsi* yenu yote.+

11 “Sasa amri hii ninayowaamuru leo si ngumu sana kwenu, wala haiko mbali msiweze kuifikia.+ 12 Haiko mbinguni, hivi kwamba mseme, ‘Ni nani atakayepanda juu mbinguni ili atuletee, tuisikie na kuishika?’+ 13 Wala haiko ng’ambo ya bahari, hivi kwamba mseme, ‘Ni nani atakayevuka ng’ambo ya bahari atuletee, tuisikie na kuishika?’ 14 Kwa maana neno hilo liko karibu sana nanyi, katika kinywa chenu wenyewe na katika moyo wenu wenyewe,+ ili mlitende.+

15 “Tazameni, naweka mbele yenu leo uzima na mema, na kifo na mabaya.+ 16 Ikiwa mtazisikiliza amri za Yehova Mungu wenu ninazowaamuru leo, kwa kumpenda Yehova Mungu wenu,+ kutembea katika njia zake, na kushika amri zake na maagizo yake na sheria zake,* basi mtaishi+ na kuongezeka, na Yehova Mungu wenu atawabariki katika nchi mnayoenda kuimiliki.+

17 “Lakini moyo wenu ukikengeuka+ na kukataa kusikiliza, mshawishiwe na kuiinamia miungu mingine na kuiabudu,+ 18 nawaambia ninyi leo kwamba hakika mtaangamia.+ Hamtaishi kwa muda mrefu katika nchi mnayovuka Yordani ili kuimiliki. 19 Nachukua mbingu na dunia kuwa mashahidi dhidi yenu leo kwamba nimeweka uzima na kifo mbele yenu, baraka na laana;+ nanyi lazima mchague uzima ili mwendelee kuishi,+ ninyi na wazao wenu,+ 20 kwa kumpenda Yehova Mungu wenu,+ kwa kuisikiliza sauti yake, na kushikamana naye,+ kwa maana yeye ni uzima wenu na kwa uwezo wake mtaishi kwa muda mrefu katika nchi ambayo Yehova aliapa kwamba angewapa mababu zenu Abrahamu, Isaka, na Yakobo.”+

31 Ndipo Musa akatoka na kuwaambia Waisraeli wote maneno haya: 2 “Leo nina umri wa miaka 120.+ Siwezi tena kuwaongoza,* kwa sababu Yehova ameniambia, ‘Hutavuka mto huu wa Yordani.’+ 3 Yehova Mungu wenu ndiye anayevuka mbele yenu, naye mwenyewe atayaangamiza mataifa haya kutoka mbele yenu, nanyi mtayafukuza.+ Yoshua ndiye atakayewaongoza kuvuka,+ kama Yehova alivyosema. 4 Yehova atayatendea kama alivyowatendea Sihoni+ na Ogu,+ wafalme wa Waamori, na nchi yao, alipowaangamiza.+ 5 Yehova atawashinda kwa niaba yenu, mtawatendea kulingana na amri yote ambayo nimewapa.+ 6 Iweni jasiri na imara.+ Msiogope wala msiwe na hofu mbele yao,+ kwa sababu Yehova Mungu wenu ndiye anayepiga mwendo pamoja nanyi. Hatawatupa wala kuwaacha.”+

7 Kisha Musa akamwita Yoshua na kumwambia hivi mbele ya Waisraeli wote: “Uwe jasiri na imara,+ kwa sababu ni wewe utakayewaingiza watu hawa katika nchi ambayo Yehova aliwaapia mababu zao kwamba atawapa, nawe utawapa iwe urithi wao.+ 8 Yehova ndiye anayepiga mwendo mbele yako, naye ataendelea kuwa pamoja nawe.+ Hatakutupa wala kukuacha. Usiogope wala usihofu.”+

9 Ndipo Musa akaandika Sheria hii+ na kuwapa makuhani, Walawi, ambao wanabeba sanduku la agano la Yehova, na wazee wote wa Israeli. 10 Musa akawaamuru hivi: “Mwishoni mwa kila miaka saba, wakati uliowekwa katika mwaka wa kufuta madeni,+ wakati wa Sherehe ya Vibanda,*+ 11 Waisraeli wote wanapokuja mbele za Yehova+ Mungu wao mahali anapochagua, unapaswa kuisoma Sheria hii mbele ya Waisraeli wote ili waisikie.+ 12 Wakusanye watu pamoja,+ wanaume, wanawake, watoto,* na mkaaji mgeni aliye katika majiji* yenu, ili wasikilize na kujifunza kumhusu Yehova Mungu wenu na kumwogopa yeye na kuwa waangalifu kutekeleza maneno yote ya Sheria hii. 13 Ndipo wana wao ambao hawajui Sheria hii watasikiliza+ na kujifunza kumwogopa Yehova Mungu wenu sikuzote ambazo mtaishi katika nchi ambayo mnavuka Yordani kuimiliki.”+

14 Kisha Yehova akamwambia Musa, “Tazama! Wakati wako wa kufa umekaribia.+ Mwite Yoshua, nanyi mwende* kwenye hema la mkutano, ili nimweke yeye kuwa kiongozi.”+ Basi Musa na Yoshua wakaenda na kusimama kwenye hema la mkutano. 15 Ndipo Yehova akatokea pale hemani katika nguzo ya wingu, na nguzo hiyo ya wingu ikasimama karibu na mlango wa hema.+

16 Sasa Yehova akamwambia Musa hivi: “Tazama! Unakaribia kufa,* na watu hawa wataanza kufanya ukahaba wa kiroho pamoja na miungu ya kigeni inayowazunguka katika nchi wanayoenda.+ Wataniacha na kuvunja agano langu+ ambalo nimefanya pamoja nao.+ 17 Wakati huo hasira yangu itawaka dhidi yao,+ nami nitawaacha+ na kuuficha uso wangu wasiuone+ mpaka watakapoangamia. Kisha baada ya kupatwa na misiba na mateso mengi,+ watasema, ‘Je, hatujapatwa na misiba hii kwa sababu Mungu wetu hayuko miongoni mwetu?’+ 18 Lakini nitaendelea kuuficha uso wangu siku hiyo kwa sababu ya maovu yote waliyotenda kwa kuigeukia miungu mingine.+

19 “Sasa jiandikieni wimbo huu+ na kuwafundisha Waisraeli.+ Hakikisheni kwamba wanajifunza wimbo huu* ili uwe ushahidi wangu dhidi ya Waisraeli.+ 20 Nitakapowaleta katika nchi ambayo niliwaapia mababu zao+—nchi inayotiririka maziwa na asali+—nao wale na kushiba na kufanikiwa,*+ wataigeukia miungu mingine na kuiabudu na kunidharau na kulivunja agano langu.+ 21 Watakapopatwa na misiba na mateso mengi,+ wimbo huu utakuwa ushahidi kwao (kwa sababu wazao wao hawapaswi kuusahau), kwa sababu tayari ninajua mwelekeo ambao wamesitawisha+ hata kabla sijawaingiza katika nchi niliyowaapia.”

22 Basi Musa akaandika wimbo huu siku hiyo na kuwafundisha Waisraeli kuuimba.

23 Kisha akamweka* Yoshua+ mwana wa Nuni kuwa kiongozi na kusema: “Uwe jasiri na imara,+ kwa sababu ni wewe utakayewaingiza Waisraeli katika nchi ambayo nimewaapia,+ nami nitaendelea kuwa pamoja nawe.”

24 Mara tu Musa alipomaliza kuandika maneno yote ya Sheria hii katika kitabu,+ 25 Musa akawaamuru hivi Walawi wanaobeba sanduku la agano la Yehova: 26 “Chukueni kitabu hiki cha Sheria+ mkiweke kando ya sanduku+ la agano la Yehova Mungu wenu, nacho kitakuwa ushahidi dhidi yenu mahali hapo. 27 Kwa maana mimi mwenyewe najua vizuri uasi wenu+ na ukaidi wenu.*+ Ikiwa mmekuwa mkimwasi sana Yehova ningali hai pamoja nanyi, basi mtamwasi kadiri gani nikifa? 28 Nikusanyieni wazee wote wa makabila yenu na maofisa wenu, acheni niwaambie maneno haya wasikie, na acheni nichukue mbingu na dunia ziwe mashahidi dhidi yao.+ 29 Kwa maana najua vizuri kwamba baada ya kifo changu hakika mtatenda maovu+ na kuacha njia ambayo nimewaamuru ninyi. Na bila shaka mtapatwa na msiba+ siku zijazo, kwa sababu mtatenda maovu machoni pa Yehova, nanyi mtamkasirisha kwa kazi za mikono yenu.”

30 Kisha mbele ya Waisraeli wote, Musa akasema maneno ya wimbo huu kuanzia mwanzo mpaka mwisho:+

32 “Sikilizeni, enyi mbingu, nami nitasema,

Dunia na isikie maneno ya kinywa changu.

 2 Mafundisho yangu yatanyesha kama mvua;

Maneno yangu yatadondoka kama umande,

Kama mvua ya rasharasha juu ya majani

Na kama manyunyu mengi juu ya mimea.

 3 Kwa maana nitalitangaza jina la Yehova.+

Nitaongea kuhusu ukuu wa Mungu wetu!+

 4 Yeye Mwamba, kazi zake ni kamilifu,+

Kwa maana njia zake zote ni haki.+

Mungu wa uaminifu+ ambaye kamwe hana ukosefu wa haki;+

Yeye ni mwadilifu na mnyoofu.+

 5 Wao ndio wametenda kwa njia ya upotovu.+

Wao si watoto wake, kasoro ni yao wenyewe.+

Wao ni kizazi kilicho kombo na kilichopotoka!+

 6 Je, hivi ndivyo mnavyopaswa kumtendea Yehova,+

Enyi watu wajinga na wasio na hekima?+

Je, yeye si Baba yenu aliyewaumba,+

Si Yeye aliyewaumba ninyi na kuwaimarisha kabisa?

 7 Kumbukeni siku za zamani;

Fikirieni miaka ya vizazi vilivyopita.

Waulizeni baba zenu, nao watawaambia;+

Wazee wenu, nao watawajulisha.

 8 Aliye Juu Zaidi alipoyapa mataifa urithi wao,+

Alipowatenganisha wana wa Adamu,*+

Aliweka mpaka wa mataifa+

Kulingana na idadi ya wana wa Israeli.+

 9 Kwa maana watu wa Yehova ni fungu lake;+

Yakobo ni urithi wake.+

10 Alimpata katika nchi yenye nyika+

Na katika jangwa tupu, lenye milio.+

Alimzunguka akimlinda, akamtunza,+

Na kumlinda kama mboni ya jicho lake.+

11 Kama tai anavyokitikisa kiota chake,

Anavyopaa juu ya makinda yake,

Akitandaza mabawa yake, na kuwachukua,

Akiwabeba juu ya mabawa yake,+

12 Yehova peke yake aliendelea kumwongoza;*+

Hakuna mungu yeyote wa kigeni aliyekuwa pamoja naye.+

13 Alimpitisha juu ya sehemu za juu za dunia,+

Hivi kwamba akala mazao ya shambani.+

Alimlisha asali kutoka katika jabali

Na mafuta kutoka katika mwamba mgumu,

14 Siagi ya mifugo na maziwa ya kundi,

Pamoja na kondoo bora,*

Na kondoo dume wa Bashani, na mbuzi dume,

Pamoja na ngano bora;*+

Nawe ulikunywa divai kutoka katika damu* ya zabibu.

15 Yeshuruni* aliponenepa, alipiga teke kwa uasi.

Umenenepa, una mafuta mengi mwilini, tumbo lako limenenepa.+

Basi akamwacha Mungu, aliyemuumba,+

Na kumdharau Mwamba wa wokovu wake.

16 Kwa miungu ya kigeni walichochea hasira yake kali;+

Walikuwa wakimkasirisha kwa mambo yanayochukiza.+

17 Walikuwa wakiwatolea dhabihu roho waovu, wala si Mungu,+

Miungu ambayo hawakuijua,

Mipya iliyokuja hivi karibuni,

Miungu ambayo mababu zenu hawakuijua.

18 Mlimsahau Mwamba,+ baba yenu aliyewazaa,

Nanyi hamkumkumbuka Mungu aliyewazaa.+

19 Yehova alipoona hilo, aliwakataa+

Kwa sababu wanawe na mabinti zake walimkasirisha.

20 Kwa hiyo akasema, ‘Nitauficha uso wangu wasiuone;+

Nitaona kitakachowapata.

Kwa maana wao ni kizazi kilichopotoka,+

Wana ambao hawana uaminifu.+

21 Wamechochea hasira yangu kali* kwa kitu ambacho si mungu;+

Wamenikasirisha kwa sanamu zao za ubatili.+

Kwa hiyo nitawachochea wawe na wivu kwa wale ambao si taifa;+

Nitawakasirisha kwa kutumia taifa lenye ujinga.+

22 Kwa maana hasira yangu imewasha moto+

Ambao utateketeza mpaka kwenye kina cha Kaburi,*+

Nao utateketeza dunia na mazao yake

Na kuchoma moto misingi ya milima.

23 Nitazidisha misiba yao;

Nitawapiga kwa mishale yangu mpaka iishe.

24 Watachoka kwa sababu ya njaa+

Na kuliwa na homa kali na maangamizi machungu.+

Nitawatumia meno ya wanyama ili yawashambulie+

Na sumu ya wanyama wanaotambaa mavumbini.

25 Nje, upanga utawaangamiza watoto wao;+

Na ndani, kuna hofu+

Kwa kijana na bikira,

Mtoto anayenyonya pamoja na mzee mwenye mvi.+

26 Ningesema: “Nitawatawanya;

Nitafanya ukumbusho wao usahauliwe kabisa miongoni mwa wanadamu,”

27 Isingekuwa kwa sababu ya kuogopa jinsi maadui wangu watakavyotenda,+

Kwa sababu huenda wapinzani wakalielewa vibaya jambo hilo.+

Huenda wakasema: “Nguvu zetu zimeshinda;+

Si Yehova aliyefanya mambo haya yote.”

28 Kwa maana wao ni taifa lisilo na akili,*

Na hawana uelewaji miongoni mwao.+

29 Laiti wangekuwa na hekima!+ Wangetafakari jambo hili.+

Wangefikiria mwisho wao.+

30 Mtu mmoja angewezaje kuwakimbiza 1,000,

Na wawili kuwafanya 10,000 wakimbie?+

Kama Mwamba wao hangekuwa amewauza+

Na Yehova kuwatia mikononi mwa maadui?

31 Kwa maana mwamba wao si kama Mwamba wetu,+

Hata maadui wetu wameelewa hilo.+

32 Kwa maana mzabibu wao unatoka katika mzabibu wa Sodoma

Na kutoka katika matuta ya Gomora.+

Zabibu zao ni zabibu za sumu,

Vishada vyao ni vichungu.+

33 Divai yao ni sumu ya nyoka,

Sumu kali ya swila.

34 Je, hili sijaliweka akibani,

Na kulifungia kabisa katika ghala langu?+

35 Kisasi ni changu, na malipo,+

Wakati utakapofika ambapo mguu wao utateleza,+

Kwa maana siku ya msiba wao iko karibu,

Na kinachowasubiri kitafika haraka.’

36 Kwa maana Yehova atawahukumu watu wake,+

Naye atawahurumia* watumishi wake+

Atakapoona nguvu zao zimeisha,

Na kwamba waliobaki ni wasio na uwezo na walio dhaifu peke yao.

37 Ndipo atakaposema, ‘Miungu yao iko wapi,+

Mwamba ambao waliukimbilia,

38 Iliyokuwa ikila mafuta ya dhabihu zao,*

Na kunywa divai ya matoleo yao ya kinywaji?+

Acheni iinuke na kuwasaidia ninyi.

Na iwe kimbilio lenu.

39 Sasa tazameni kwamba mimi—mimi ndiye,+

Na hakuna miungu mingine ila mimi.+

Mimi huua, nami hufanya kuwa hai.+

Ninajeruhi,+ nami nitaponya,+

Na hakuna anayeweza kumwokoa yeyote kutoka mikononi mwangu.+

40 Kwa maana nainua mkono wangu mbinguni,

Na kuapa hivi: “Kwa hakika kama niishivyo milele,”+

41 Nikiunoa upanga wangu unaometameta

Na kuutayarisha mkono wangu ili uhukumu,+

Nitawalipiza kisasi maadui wangu+

Na kuwalipa wale wanaonichukia.

42 Nitailewesha mishale yangu kwa damu,

Na upanga wangu utakula nyama,

Pamoja na damu ya waliouawa na pia mateka,

Pamoja na vichwa vya viongozi wa adui.’

43 Furahini, enyi mataifa, pamoja na watu wake,+

Kwa maana atailipizia kisasi damu ya watumishi wake,+

Atawalipiza kisasi maadui wake+

Na kufunika dhambi ya* nchi ya watu wake.”

44 Basi Musa akaja na kuyasema maneno yote ya wimbo huo watu wakisikia;+ alikuwa na Hoshea*+ mwana wa Nuni. 45 Musa alipomaliza kuwaambia Waisraeli wote maneno hayo yote, 46 akawaambia hivi: “Wekeni mioyoni mwenu maonyo yote niliyowapa leo,+ ili muwaamuru wana wenu wawe waangalifu kutenda maneno yote ya Sheria hii.+ 47 Kwa maana haya si maneno matupu kwenu, bali yanamaanisha uhai wenu,+ na kwa maneno haya mnaweza kuishi kwa muda mrefu katika nchi ambayo mnavuka Yordani kuimiliki.”

48 Yehova akaongea na Musa siku hiyohiyo na kumwambia hivi: 49 “Panda juu ya mlima huu wa Abarimu,+ Mlima Nebo,+ ulio katika nchi ya Moabu, unaoelekeana na Yeriko, nawe utazame nchi ya Kanaani, ninayowapa Waisraeli waimiliki.+ 50 Kisha utakufa juu ya mlima utakaopanda hivi punde, na kuzikwa pamoja na watu wako,* kama Haruni ndugu yako alivyokufa juu ya Mlima Hori+ na kuzikwa pamoja na watu wake, 51 kwa sababu nyote wawili hamkuwa waaminifu kwangu miongoni mwa Waisraeli kwenye maji ya Meriba+ kule Kadeshi katika nyika ya Zini, kwa sababu hamkunitakasa mbele ya Waisraeli.+ 52 Utaiona nchi hiyo kwa mbali, lakini hutaingia katika nchi hiyo ninayowapa Waisraeli.”+

33 Sasa hii ndiyo baraka ambayo Musa mtu wa Mungu wa kweli aliwatangazia Waisraeli kabla ya kifo chake.+ 2 Alisema hivi:

“Yehova—alikuja kutoka Sinai,+

Naye akawaangazia kutoka Seiri.

Aliangaza kwa utukufu kutoka katika eneo lenye milima la Parani,+

Naye alikuwa pamoja na makumi ya maelfu ya watakatifu,+

Na mashujaa wake kwenye mkono wake wa kuume.+

 3 Aliwapenda watu wake;+

Watakatifu wao wote wako mikononi mwako.+

Waliketi miguuni pako;+

Walianza kusikiliza maneno yako.+

 4 (Musa alitupatia amri, sheria,+

Kuwa miliki ya kutaniko la Yakobo.)+

 5 Naye akawa mfalme kule Yeshuruni,*+

Viongozi wa watu walipokusanyika pamoja,+

Pamoja na makabila yote ya Israeli.+

 6 Rubeni na aishi wala asife,+

Na watu wake wasiwe wachache.”+

 7 Naye akamtangazia Yuda baraka hii:+

“Ee Yehova, isikie sauti ya Yuda,+

Nawe umrudishe kwa watu wake.

Mikono yake imetetea* kilicho chake,

Nawe umsaidie dhidi ya maadui wake.”+

 8 Akasema hivi kumhusu Lawi:+

“Thumimu yako* na Urimu+ yako ni vya mtu aliye mshikamanifu kwako,+

Uliyemjaribu kule Masa.+

Ulianza kupambana naye karibu na maji ya Meriba,+

 9 Mtu aliyemwambia baba yake na mama yake, ‘Sijawaheshimu.’

Hata ndugu zake hakuwatambua,+

Na watoto wake mwenyewe aliwapuuza.

Kwa maana walitii neno lako,

Na kulishika agano lako.+

10 Acha wamfundishe Yakobo amri zako*+

Na Waisraeli Sheria yako.+

Acha wakufukizie uvumba wenye harufu inayokupendeza*+

Na dhabihu nzima ya kuteketezwa kwenye madhabahu yako.+

11 Ee Yehova, bariki nguvu zake,

Na ufurahie kazi ya mikono yake.

Ivunje miguu ya* wale wanaoinuka dhidi yake,

Ili wale wanaomchukia wasiinuke tena.”

12 Alisema hivi kumhusu Benjamini:+

“Mwache mpendwa wa Yehova akae kwa usalama kando yake;

Akimkinga siku nzima,

Atakaa katikati ya mabega yake.”

13 Alisema hivi kumhusu Yosefu:+

“Nchi yake na ibarikiwe na Yehova+

Kwa vitu bora vya mbinguni,

Kwa umande na maji kutoka katika chemchemi zilizo chini,+

14 Kwa vitu bora vinavyoletwa na jua

Na mazao bora kila mwezi,+

15 Kwa vitu bora kabisa kutoka katika milima ya zamani*+

Na vitu bora kutoka katika vilima vinavyodumu,

16 Kwa vitu bora vya dunia na vitu vinavyoijaza,+

Na kwa kibali cha Yule anayekaa katika kichaka cha miiba.+

Na vije juu ya kichwa cha Yosefu,

Juu ya utosi wa kichwa cha yule aliyechaguliwa kutoka kati ya ndugu zake.+

17 Fahari yake ni kama ya mzaliwa wa kwanza wa ng’ombe dume,

Na pembe zake ni pembe za fahali mwitu.

Atazitumia kuyasukuma* mataifa

Yote pamoja mpaka miisho ya dunia.

Wao ni makumi ya maelfu ya Efraimu,+

Nao ni maelfu ya Manase.”

18 Alisema hivi kumhusu Zabuloni:+

“Shangilia, Ee Zabuloni, unapotoka nje,

Nawe, Isakari, katika mahema yako.+

19 Watayaita mataifa mlimani.

Huko watatoa dhabihu za uadilifu.

Kwa maana watafyonza* utajiri mwingi wa bahari

Na marundo yaliyofichika* mchangani.”

20 Alisema hivi kumhusu Gadi:+

“Amebarikiwa yule anayepanua mipaka ya Gadi.+

Analala huko kama simba,

Akiwa tayari kuunyafua mkono, naam, utosi wa kichwa.

21 Atajichagulia fungu la kwanza,+

Kwa maana huko fungu la mpaji sheria limehifadhiwa.+

Viongozi wa watu watakusanyika pamoja.

Uadilifu wa Yehova atautekeleza,

Na amri zake* pamoja na Israeli.”

22 Alisema hivi kumhusu Dani:+

“Dani ni mwanasimba.+

Ataruka kutoka Bashani.”+

23 Alisema hivi kumhusu Naftali:+

“Naftali ameshiba kibali

Naye amejaa baraka ya Yehova.

Imiliki magharibi na kusini.”

24 Alisema hivi kumhusu Asheri:+

“Asheri amebarikiwa kuwa na wana.

Na apendwe na ndugu zake,

Naye achovye* miguu yake katika mafuta.

25 Makufuli ya lango lako ni chuma na shaba,+

Nawe utakuwa salama siku zako zote.*

26 Hakuna aliye kama Mungu wa kweli+ wa Yeshuruni,+

Anayepita mbinguni kuja kukusaidia

Na kupita juu ya mawingu katika fahari yake.+

27 Mungu ni kimbilio tangu nyakati za kale,+

Mikono yake ya milele iko chini yako.+

Naye atamfukuza adui kutoka mbele yako,+

Naye atasema, ‘Waangamize!’+

28 Israeli atakaa kwa usalama,

Na chemchemi ya Yakobo itatengwa peke yake

Katika nchi ya nafaka na divai mpya,+

Na anga lake litadondosha umande.+

29 Wewe ni mwenye furaha, Ee Israeli!+

Ni nani aliye kama wewe,+

Taifa linalofurahia wokovu wa Yehova,+

Ngao yenu inayowalinda+

Na upanga wenu wenye fahari?

Maadui wenu watajikunyata mbele yenu,+

Nanyi mtawakanyaga migongoni.”*

34 Kisha Musa akatoka katika jangwa tambarare la Moabu na kupanda Mlima Nebo,+ kwenye kilele cha Pisga,+ kinachoelekeana na Yeriko.+ Yehova akamwonyesha nchi yote, kuanzia Gileadi mpaka Dani,+ 2 na nchi yote ya Naftali na nchi ya Efraimu na Manase, na nchi yote ya Yuda mpaka bahari ya magharibi,*+ 3 na Negebu+ na ile Wilaya,+ bonde tambarare la Yeriko, jiji la mitende, mpaka Soari.+

4 Kisha Yehova akamwambia hivi: “Hii ndiyo nchi ambayo nilimwapia Abrahamu, Isaka, na Yakobo, niliposema, ‘Nitaupa uzao wako* nchi hii.’+ Nimekuruhusu uione kwa macho yako mwenyewe, lakini hutavuka kuingia humo.”+

5 Kisha Musa mtumishi wa Yehova akafa huko katika nchi ya Moabu kama Yehova alivyosema.+ 6 Akamzika bondeni katika nchi ya Moabu, ng’ambo ya Beth-peori, na hakuna mtu anayejua kaburi lake liko wapi mpaka leo hii.+ 7 Musa alikuwa na umri wa miaka 120 alipokufa.+ Macho yake hayakuwa yamedhoofika, na nguvu zake hazikuwa zimeisha. 8 Waisraeli walimlilia Musa katika jangwa tambarare la Moabu kwa siku 30.+ Kisha siku za kumlilia na kumwombolezea Musa zikaisha.

9 Yoshua mwana wa Nuni alikuwa amejaa roho ya hekima, kwa kuwa Musa alikuwa ameweka mkono wake juu yake;+ na Waisraeli wakaanza kumsikiliza, nao wakafanya kama Yehova alivyokuwa amemwamuru Musa.+ 10 Lakini hajatokea tena nabii mwingine katika Israeli aliye kama Musa,+ ambaye Yehova alimjua uso kwa uso.+ 11 Alifanya ishara zote na miujiza ambayo Yehova alimtuma afanye katika nchi ya Misri kwa Farao na watumishi wake wote na nchi yake yote,+ 12 pamoja na mkono wenye nguvu na nguvu zinazoogopesha ambazo Musa alidhihirisha machoni pa Waisraeli wote.+

Tnn., “wana wa Israeli.”

Inaonekana ni safu ya milima ya Lebanoni.

Tnn., “mbegu yao.”

Tnn., “walifanya moyo wetu uyeyuke.”

Yaani, yana kuta ndefu sana.

Tnn., “kikamilifu; kabisa.”

Tnn., “anayesimama mbele yako.”

Au labda, “Mungu amemwimarisha.”

Au “Msiwachokoze.”

Au “Korongo.”

Yaani, Krete.

Au “Korongo.”

Tnn., “walio chini ya mbingu.”

Au “watakuwa na uchungu kama wa kuzaa.”

Au “Korongo.”

Au “Korongo.”

Au “Korongo.”

Au “jiwe jeusi la volkano.”

Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.

Au “Korongo.”

Maana yake “Vijiji vya Mahema vya Yairi.”

Au “Korongo.”

Tnn., “maamuzi ya hukumu ambayo.”

Tnn., “maamuzi ya hukumu.”

Tnn., “maamuzi ya hukumu.”

Tnn., “yale Maneno Kumi.”

Tnn., “maamuzi ya hukumu ambayo.”

Tnn., “walio chini ya mbingu.”

Au “urithi wake.”

Angalia Kamusi.

Au “majaribu.”

Tnn., “mbegu yao.”

Tnn., “maamuzi ya hukumu ambayo.”

Yaani, Bahari ya Chumvi.

Tnn., “maamuzi ya hukumu ambayo.”

Au “dhidi yangu.” Tnn., “dhidi ya uso wangu.”

Au “umbo la.”

Au “fadhili zenye upendo.”

Tnn., “malango.”

Au “na ili mambo yakuendee vyema.”

Tnn., “maneno hayo.”

Au “ni nani mwenye mwili wa nyama.”

Angalia Kamusi.

Au “uwezo wako wote.”

Au “uyarudie; uyasisitize.”

Tnn., “katikati ya macho yako.”

Tnn., “maamuzi ya hukumu.”

Angalia Kamusi.

Au “mali yake anayothamini sana.”

Tnn., “kutoka mikononi mwa.”

Tnn., “mbele ya uso wao.”

Tnn., “mbele ya uso wao.”

Tnn., “maamuzi ya hukumu ambayo.”

Tnn., “atabariki uzao wa tumbo lenu.”

Tnn., “Mtayameza.”

Tnn., “Jicho lenu lisiwahurumie.”

Au “yale majaribu makubwa.”

Au labda, “washikwe na wasiwasi; waogope.”

Tnn., “kutoka chini ya mbingu.”

Au “vyanzo vya maji vyenye kina kirefu.”

Yaani, yana kuta ndefu sana.

Au “mchukue nchi yao.”

Tnn., “wenye shingo ngumu.”

Au “kukutanika.”

Au “sanamu ya kuyeyushwa.”

Au “wenye shingo ngumu.”

Tnn., “kutoka chini ya mbingu.”

Au “kuyeyushwa.”

Au “urithi wako.”

Au “urithi wako.”

Tnn., “yale Maneno Kumi.”

Au “kukutanika.”

Angalia Kamusi.

Au “mbingu zilizo juu zaidi.”

Tnn., “mtahiri govi la.”

Au “mwache kufanya shingo zenu kuwa ngumu.”

Au “nafsi.”

Au “mpaka leo.”

Tnn., “mbegu yao.”

Yaani, kwa kutumia mfumo fulani uliokanyagwa kwa mguu, labda mfumo unaotumia gurudumu la maji au kwa kuchimba na kufungua mitaro ya maji kwa miguu.

Angalia Kamusi.

Yaani, Mungu.

Angalia Kamusi.

Tnn., “katikati ya macho yako.”

Yaani, ile Bahari Kuu, Mediterania.

Au “machweo ya jua.”

Tnn., “maamuzi yote ya hukumu ninayoweka.”

Angalia Kamusi.

Au “analofikiri linafaa.”

Tnn., “malango.”

Tnn., “ndani ya malango.”

Tnn., “malango.”

Tnn., “malango.”

Au “nafsi zenu zinatamani.”

Tnn., “malango.”

Au “nafsi.”

Au “nafsi.”

Angalia Kamusi.

Au “rafiki yako ambaye ni kama nafsi yako mwenyewe.”

Au “kilichofanywa kitakatifu kwa kupigwa marufuku.”

Au “kusikiliza sauti ya.”

Tnn., “kutia (kunyoa) upara katikati ya macho yenu.”

Au “mali yake anayothamini sana.”

Au “tai mla mizoga.”

Au “mdudu.”

Tnn., “malango.”

Au “kumkopesha kwa rehani.”

Tnn., “moyo wenu haupaswi.”

Tnn., “malango.”

Angalia Nyongeza B15.

Tnn., “malango.”

Au “Vibanda vya Muda.”

Au “Vibanda vya Muda.”

Angalia Kamusi.

Tnn., “kinywa cha.”

Tnn., “kumwaga damu.”

Au “hati ya kukunjwa.”

Yaani, mahali ambapo Yehova anachagua kuwa kitovu cha ibada.

Tnn., “anayempitisha.”

Au “anayebashiri.”

Au “ubashiri.”

Au “kukutanika.”

Tnn., “Jicho lenu lisimhurumie.”

Tnn., “kinywa cha.”

Tnn., “Jicho lenu halipaswi.”

Tnn., “Nafsi itatolewa kwa nafsi.”

Au “asifanye mioyo ya ndugu zake iyeyuke kama moyo wake mwenyewe.”

Au “korongo.”

Tnn., “wake wawili, mmoja anayependwa na mwingine anayechukiwa.”

Au “amkatae.”

Au “anamkataa.”

Au “ukahaba.”

Tnn., “kumchukua.”

Tnn., “asimfunue nguo baba yake.”

Au “kinachochafua.”

Yaani, choo.

Au “malipo.” Tnn., “bei.”

Tnn., “mbwa.”

Au “akimkataa.”

Au “rehani.”

Au “kuchukua uhai wa; kuchukua nafsi ya.”

Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “ukoma” lina maana pana na linaweza kutia ndani magonjwa mbalimbali ya ngozi yanayoambukiza. Linaweza pia kutia ndani maambukizi fulani yaliyopatikana kwenye nguo na nyumba.

Tnn., “malango.”

Au “nafsi yake inategemea.”

Au “rehani.”

Au “jina la nyumba.” Tnn., “jina lake.”

Tnn., “Nyumba.”

Tnn., “Jicho lenu halipaswi.”

Tnn., “efa na efa.” Angalia Nyongeza B14.

Tnn., “matunda.”

Au labda, “akiangamia.”

Tnn., “malango.”

Tnn., “maamuzi haya ya hukumu.”

Angalia Kamusi.

Tnn., “maamuzi yake ya hukumu.”

Au “mali yake anayothamini sana.”

Au “kuyapiga lipu.”

Au “kuyapiga lipu.”

Au “sanamu ya kuyeyushwa.”

Au “fundi wa mbao na chuma.”

Au “Na iwe hivyo!”

Tnn., “amemfunua nguo baba yake.”

Tnn., “Wazao wa tumbo lenu.”

Tnn., “Wazao wa tumbo lenu.”

Au “mvurugike moyoni.”

Tnn., “methali.”

Au “Wadudu wanaoruka.”

Au “bila kitu chochote.”

Tnn., “malango.”

Tnn., “wazao wa tumbo lenu.”

Au “nafsi iliyokata tamaa.”

Au “majaribu makubwa ambayo.”

Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.

Tnn., “kitu kilichonyweshwa maji vizuri pamoja na kitu kilichokauka.”

Tnn., “chini ya mbingu.”

Au “hakuwapa.”

Tnn., “myatie tena moyoni mwenu.”

Angalia Kamusi.

Tnn., “ataitahiri.”

Angalia Kamusi.

Angalia Kamusi.

Tnn., “maamuzi yake ya hukumu.”

Tnn., “kutoka nje na kuingia ndani.”

Au “Vibanda vya Muda.”

Tnn., “watoto wachanga.”

Tnn., “malango.”

Au “mchukue nafasi zenu.”

Tnn., “kulala na baba zako.”

Tnn., “Utieni katika vinywa vyao.”

Tnn., “kunenepa.”

Inaonekana ni Mungu.

Tnn., “shingo yenu ngumu.”

Au labda, “Alipoitenganisha jamii ya wanadamu.”

Yaani, Yakobo.

Tnn., “mafuta ya kondoo.”

Tnn., “mafuta ya figo ya ngano.”

Au “maji.”

Maana yake “Mnyoofu,” jina la heshima la Israeli.

Au “wivu wangu.”

Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.

Au labda, “lisilosikia ushauri.”

Au “ataghairi kwa sababu ya.”

Au “kula dhabihu zao bora.”

Au “Na kuisafisha.”

Jina la awali la Yoshua. Hoshea ni ufupisho wa jina Hoshaya, linalomaanisha “Aliyeokolewa na Yah; Yah Ameokoa.”

Tnn., “kukusanywa kwa watu wako.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.

Maana yake “Mnyoofu,” jina la heshima la Israeli.

Au “imepigania.”

Neno “yako” katika mstari huu linamrejelea Mungu.

Tnn., “maamuzi yako ya hukumu.”

Tnn., “inayopendeza puani mwako.”

Au “Vivunje viuno vya.”

Au labda, “milima ya mashariki.”

Au “kuyapiga.”

Tnn., “watanyonya.”

Au “hazina zilizofichika.”

Tnn., “maamuzi yake ya hukumu.”

Au “anawe.”

Tnn., “Kama zilivyo siku zako ndivyo zitakavyokuwa nguvu zako.”

Au labda, “mtakanyaga mahali pao pa juu.”

Yaani, ile Bahari Kuu, Mediterania.

Tnn., “Nitaipa mbegu yako.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki