Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt Mambo ya Walawi 1:1-27:34
  • Mambo ya Walawi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mambo ya Walawi
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Mambo ya Walawi

MAMBO YA WALAWI

1 Na Yehova akamwita Musa na kuzungumza naye katika hema la mkutano,+ akamwambia: 2 “Zungumza na Waisraeli* uwaambie, ‘Ikiwa yeyote kati yenu atamtolea Yehova mnyama wa kufugwa, anapaswa kumtolea dhabihu kutoka kati ya mifugo yake au kundi lake.+

3 “‘Ikiwa anatoa dhabihu ya kuteketezwa kutoka kati ya mifugo yake, anapaswa kutoa mnyama dume asiye na kasoro.+ Atamtoa kwa hiari yake mwenyewe+ mbele za Yehova kwenye mlango wa hema la mkutano. 4 Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha dhabihu hiyo ya kuteketezwa, nayo itakubaliwa kwa niaba yake ili kufunika dhambi zake.

5 “‘Kisha huyo ng’ombe dume mchanga atachinjwa mbele za Yehova, nao wana wa Haruni, makuhani,+ wataleta damu ya mnyama huyo na kuinyunyiza pande zote za madhabahu,+ kwenye mlango wa hema la mkutano. 6 Mnyama huyo wa dhabihu ya kuteketezwa anapaswa kuchunwa ngozi na kukatwa vipandevipande.+ 7 Wana wa Haruni, makuhani, wataweka moto kwenye madhabahu+ na kupanga kuni kwenye moto huo. 8 Wana wa Haruni, makuhani, watapanga vile vipande vya mnyama wa dhabihu+ pamoja na kichwa na mafuta yanayofunika figo juu ya kuni kwenye moto wa madhabahu. 9 Matumbo na miguu yake itaoshwa kwa maji, na kuhani atachoma moto vitu hivyo vyote ili vifuke moshi kwenye madhabahu. Ni dhabihu ya kuteketezwa, dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova.+

10 “‘Ikiwa anatoa dhabihu kutoka katika kundi,+ yaani, kutoka kati ya wanakondoo dume au mbuzi, anapaswa kutoa dume asiye na kasoro.+ 11 Atachinjiwa upande wa kaskazini wa madhabahu mbele za Yehova, nao wana wa Haruni, makuhani, watanyunyiza damu yake pande zote za madhabahu.+ 12 Atamkata vipandevipande, naye kuhani atavipanga vipande hivyo pamoja na kichwa na mafuta yaliyo kwenye figo juu ya kuni kwenye moto wa madhabahu. 13 Ataosha matumbo na miguu yake kwa maji, kisha kuhani atavileta vyote na kuvichoma moto ili vifuke moshi kwenye madhabahu. Ni dhabihu ya kuteketezwa, dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova.

14 “‘Hata hivyo, ikiwa anamtoa ndege kuwa dhabihu ya kuteketezwa kwa Yehova, atamtoa njiwa tetere au hua mchanga.+ 15 Kuhani atamtoa kwenye madhabahu, atamvunja shingo na kuacha kichwa kikining’inia, kisha atamchoma moto juu ya madhabahu ili afuke moshi, lakini damu yake itamwagwa kando ya madhabahu. 16 Ataondoa kifuko cha chakula kilicho kooni mwake pamoja na manyoya yake na kuvitupa vitu hivyo kando ya madhabahu, upande wa mashariki, mahali panapowekwa majivu.*+ 17 Atampasua kwenye mabawa yake bila kumkata vipande viwili. Kisha kuhani atamchoma moto juu ya kuni zilizo kwenye madhabahu ili afuke moshi. Ni dhabihu ya kuteketezwa, dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova.

2 “‘Sasa ikiwa mtu atamtolea Yehova toleo la nafaka,+ ni lazima toleo lake liwe la unga laini, naye anapaswa kumimina mafuta juu yake na kuweka ubani juu yake.+ 2 Kisha atalipeleka kwa wana wa Haruni, makuhani, naye kuhani atachukua mkono mmoja wa unga huo laini, mafuta, pamoja na ubani wake wote, naye atauteketeza ili ufuke moshi ikiwa dhabihu ya kumbukumbu*+ juu ya madhabahu. Ni dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova. 3 Chochote kinachobaki cha toleo hilo la nafaka kitakuwa cha Haruni na wanawe,+ kitakuwa kitu kitakatifu kabisa+ kutoka kwa dhabihu za Yehova zinazochomwa kwa moto.

4 “‘Mkitoa nafaka ambayo imeokwa kwenye jiko, inapaswa kuwa ya unga laini, mikate ya mviringo isiyo na chachu na iliyokandwa kwa mafuta, au mikate myembamba isiyo na chachu ambayo imepakwa mafuta.+

5 “‘Mkitoa toleo la nafaka kutoka katika kiokeo,+ inapaswa kuwa ya unga laini usio na chachu, uliokandwa kwa mafuta. 6 Toleo hilo litavunjwa vipandevipande na mafuta yatamiminwa juu yake.+ Ni toleo la nafaka.

7 “‘Mkitoa toleo la nafaka iliyokaangwa kwenye kikaangio, linapaswa kuwa la unga laini uliokandwa kwa mafuta. 8 Mnapaswa kumletea Yehova toleo la nafaka lililotengenezwa kwa vitu hivyo, nalo litapelekwa kwa kuhani ambaye atalipeleka karibu na madhabahu. 9 Naye kuhani atachukua sehemu ya toleo hilo la nafaka ikiwa dhabihu ya kumbukumbu*+ na kuiteketeza juu ya madhabahu ili ifuke moshi. Ni dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova.+ 10 Chochote kinachobaki cha toleo hilo la nafaka kitakuwa cha Haruni na wanawe, kitakuwa kitu kitakatifu kabisa kutoka kwa dhabihu za Yehova zinazoteketezwa.+

11 “‘Toleo lolote la nafaka mnalomtolea Yehova halipaswi kutiwa chachu,+ kwa maana hampaswi kuuteketeza unga wowote uliokandwa ulio na chachu au kuiteketeza asali ili ifuke moshi ikiwa toleo la Yehova linalochomwa kwa moto.

12 “‘Mnaweza kumtolea Yehova vitu hivyo vikiwa mazao ya kwanza,+ lakini hampaswi kuvileta kwenye madhabahu vikiwa dhabihu ya kuteketezwa yenye harufu inayopendeza.*

13 “‘Kila toleo la nafaka mnalotoa linapaswa kukolezwa kwa chumvi; na msiruhusu kamwe chumvi ya agano la Mungu wenu ikosekane katika toleo lenu la nafaka. Kila toleo mtakalotoa, mtalitoa pamoja na chumvi.+

14 “‘Mkimtolea Yehova mavuno ya kwanza ya nafaka iliyokomaa yakiwa toleo la nafaka, mnapaswa kutoa masuke mabichi yaliyokaangwa kwa moto, chengachenga za nafaka mbichi iliyopondwa, kuwa toleo la nafaka la mavuno yenu ya kwanza yaliyokomaa.+ 15 Mnapaswa kutia mafuta na ubani juu yake. Ni toleo la nafaka. 16 Kuhani ataiteketeza ikiwa dhabihu ya kumbukumbu*+ ili ifuke moshi, yaani, baadhi ya chengachenga za nafaka pamoja na mafuta na ubani wake wote. Ni dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto.

3 “‘Ikiwa mtu anatoa dhabihu ya ushirika*+ na dhabihu hiyo inatoka kati ya mifugo, awe ni mnyama dume au jike, anapaswa kumtolea Yehova mnyama asiye na kasoro. 2 Anapaswa kuweka mkono wake juu ya kichwa cha mnyama huyo, naye atachinjwa kwenye mlango wa hema la mkutano; kisha wana wa Haruni, makuhani, watanyunyiza damu yake pande zote za madhabahu. 3 Atatoa sehemu ya dhabihu hiyo ya ushirika kuwa dhabihu kwa Yehova+ inayochomwa kwa moto, yaani, mafuta+ yanayofunika matumbo, naam, mafuta yote yaliyo juu ya matumbo, 4 na figo zake mbili pamoja na mafuta yake yaliyo karibu na kiuno. Ataondoa pia figo pamoja na mafuta yaliyo juu ya ini.+ 5 Wana wa Haruni watateketeza vitu hivyo kwenye madhabahu juu ya dhabihu ya kuteketezwa iliyo kwenye kuni zinazowaka moto ili vifuke moshi;+ ni dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova.+

6 “‘Ikiwa mtu anamtolea Yehova dhabihu ya ushirika kutoka kati ya kundi lake, anapaswa kutoa mnyama dume au jike asiye na kasoro.+ 7 Ikiwa anatoa kondoo dume mchanga, atamtoa mbele za Yehova. 8 Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha mnyama huyo, naye atachinjwa mbele ya hema la mkutano. Kisha wana wa Haruni, makuhani, watanyunyiza damu yake pande zote za madhabahu. 9 Atayatoa mafuta kutoka kwenye dhabihu ya ushirika yawe dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto.+ Atakata mkia wote wenye mafuta karibu na uti wa mgongo, ataondoa mafuta yanayofunika matumbo, naam, mafuta yote yaliyo juu ya matumbo, 10 na figo zake mbili pamoja na mafuta yake yaliyo karibu na kiuno. Ataondoa pia figo pamoja na mafuta yaliyo juu ya ini.+ 11 Naye kuhani ataviteketeza vitu hivyo kwenye madhabahu kama chakula* ili vifuke moshi. Ni dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto.+

12 “‘Ikiwa mtu anatoa mbuzi, atamtoa mbele za Yehova. 13 Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha mbuzi huyo, naye atachinjwa mbele ya hema la mkutano, nao wana wa Haruni watanyunyiza damu yake pande zote za madhabahu. 14 Atamtolea Yehova mafuta yanayofunika matumbo, naam, mafuta yote yaliyo juu ya matumbo kuwa dhabihu inayochomwa kwa moto,+ 15 pamoja na figo zake mbili na mafuta yake yaliyo karibu na kiuno. Ataondoa pia figo pamoja na mafuta yaliyo juu ya ini. 16 Kuhani ataviteketeza vitu hivyo kwenye madhabahu kama chakula* ili vifuke moshi, ni dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayopendeza.* Mafuta yote ni ya Yehova.+

17 “‘Ni sheria ya kudumu kwa vizazi vyenu, katika makao yenu yote: Msile mafuta yoyote wala damu+ yoyote.’”

4 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Waambie Waisraeli, ‘Mtu akitenda dhambi bila kukusudia+ kwa kufanya jambo lolote ambalo Yehova ameamuru lisifanywe:

3 “‘Kuhani aliyetiwa mafuta+ akitenda dhambi+ na kuwaletea watu hatia, basi atamtolea Yehova ng’ombe dume mchanga asiye na kasoro, kuwa dhabihu ya dhambi kwa ajili ya dhambi aliyotenda.+ 4 Atamleta huyo ng’ombe dume kwenye mlango wa hema la mkutano+ mbele za Yehova na kuweka mkono wake juu ya kichwa cha ng’ombe dume huyo, naye atamchinja mbele za Yehova.+ 5 Kisha kuhani aliyetiwa mafuta+ atachukua kiasi fulani cha damu ya ng’ombe dume huyo na kuileta ndani ya hema la mkutano; 6 naye atachovya kidole chake ndani ya damu+ hiyo na kunyunyiza kiasi fulani mara saba+ mbele za Yehova, mbele ya pazia la mahali patakatifu. 7 Pia, kuhani atatia kiasi fulani cha damu hiyo kwenye pembe za madhabahu ya uvumba uliotiwa manukato,+ mbele za Yehova katika hema la mkutano; naye atamwaga damu yote iliyobaki ya huyo ng’ombe dume kwenye msingi wa madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa,+ kwenye mlango wa hema la mkutano.

8 “‘Kisha ataondoa mafuta yote ya huyo ng’ombe dume wa dhabihu ya dhambi, pamoja na mafuta yanayofunika matumbo na mafuta yanayozunguka matumbo, 9 na figo zake mbili pamoja na mafuta yake yaliyo karibu na kiuno. Ataondoa pia figo pamoja na mafuta yaliyo juu ya ini.+ 10 Ataondoa sehemu zilezile zinazoondolewa katika ng’ombe dume wa dhabihu ya ushirika.+ Na kuhani ataviteketeza kwenye madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa ili vifuke moshi.

11 “‘Lakini ngozi ya ng’ombe dume huyo na nyama yake yote pamoja na kichwa chake, miguu yake, matumbo yake, na mavi yake+— 12 sehemu zote zinazobaki za ng’ombe dume huyo—atazipeleka mahali safi nje ya kambi, mahali ambapo majivu* hutupwa, naye ataziteketeza kwa moto juu ya kuni.+ Zinapaswa kuteketezwa mahali ambapo majivu hutupwa.

13 “‘Sasa ikiwa kusanyiko lote la Waisraeli lina hatia ya kutenda dhambi bila kukusudia,+ lakini halikujua kwamba limefanya jambo ambalo Yehova aliamuru lisifanywe,+ 14 kisha dhambi hiyo ijulikane, ni lazima kusanyiko litoe ng’ombe dume mchanga kwa ajili ya dhabihu ya dhambi na kumleta mbele ya hema la mkutano. 15 Wazee wa kusanyiko hilo wataweka mikono yao juu ya kichwa cha ng’ombe dume huyo mbele za Yehova, naye atachinjwa mbele za Yehova.

16 “‘Kisha kuhani aliyetiwa mafuta ataleta kiasi fulani cha damu ya ng’ombe dume huyo katika hema la mkutano. 17 Naye atachovya kidole chake ndani ya damu hiyo na kunyunyiza kiasi fulani mara saba mbele za Yehova, mbele ya pazia.+ 18 Kisha atatia kiasi fulani cha damu hiyo kwenye pembe za madhabahu+ iliyo mbele za Yehova, katika hema la mkutano; naye atamwaga damu yote iliyobaki kwenye msingi wa madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa, iliyo kwenye mlango wa hema la mkutano.+ 19 Ataondoa mafuta yake yote na kuyateketeza kwenye madhabahu ili yafuke moshi.+ 20 Atamfanya ng’ombe dume huyo kama alivyomfanya yule ng’ombe dume wa dhabihu ya dhambi. Hivyo ndivyo atakavyomfanya, kuhani atatoa dhabihu ya kufunika dhambi zao,+ nao watasamehewa. 21 Atampeleka ng’ombe dume huyo nje ya kambi na kumteketeza kama alivyomteketeza ng’ombe dume wa kwanza.+ Ni dhabihu ya dhambi kwa ajili ya kusanyiko lote.+

22 “‘Ikiwa mkuu+ ametenda dhambi bila kukusudia na hivyo ana hatia ya kufanya jambo lolote ambalo Yehova Mungu wake ameamuru lisifanywe, 23 au akigundua dhambi aliyotenda kinyume cha amri, basi anapaswa kumleta mwanambuzi dume asiye na kasoro ili atolewe dhabihu kwa ajili yake. 24 Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha mwanambuzi huyo na kumchinjia mahali ambapo dhabihu za kuteketezwa huchinjwa mbele za Yehova.+ Hiyo ni dhabihu ya dhambi. 25 Kuhani atachukua kwa kidole chake kiasi kidogo cha damu ya dhabihu ya dhambi na kuitia kwenye pembe+ za madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa, naye atamwaga damu inayobaki kwenye msingi wa madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa.+ 26 Naye atayateketeza mafuta yake yote kwenye madhabahu ili yafuke moshi kama yale mafuta ya dhabihu ya ushirika;+ naye kuhani atatoa dhabihu ya kufunika dhambi ya mtu huyo, naye atasamehewa.

27 “‘Mtu yeyote miongoni mwa watu walio nchini akitenda dhambi bila kukusudia na hivyo kuwa na hatia ya kufanya jambo lolote ambalo Yehova ameamuru lisifanywe,+ 28 au akigundua dhambi aliyotenda, basi atamleta mwanambuzi jike asiye na kasoro ili atolewe dhabihu kwa ajili ya dhambi aliyotenda. 29 Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha mnyama wa dhabihu ya dhambi na kumchinjia mahali ambapo dhabihu za kuteketezwa huchinjwa.+ 30 Kuhani atachukua kwa kidole chake kiasi kidogo cha damu ya mnyama huyo na kuitia kwenye pembe za madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa, naye atamwaga damu yote inayobaki kwenye msingi wa madhabahu.+ 31 Ataondoa mafuta yake yote+ kama mafuta ya dhabihu ya ushirika+ yanavyoondolewa, na kuhani atayateketeza kwenye madhabahu ili yafuke moshi yakiwa harufu inayompendeza* Yehova; naye kuhani atatoa dhabihu ya kufunika dhambi ya mtu huyo, naye atasamehewa.

32 “‘Lakini akitoa mwanakondoo ili awe dhabihu yake ya dhambi, anapaswa kuleta mwanakondoo jike asiye na kasoro. 33 Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha mnyama wa dhabihu ya dhambi na kumchinjia mahali ambapo dhabihu za kuteketezwa huchinjwa.+ 34 Kuhani atachukua kwa kidole chake kiasi kidogo cha damu ya mnyama huyo na kuitia kwenye pembe za madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa,+ naye atamwaga damu yote inayobaki kwenye msingi wa madhabahu. 35 Ataondoa mafuta yake yote kama mafuta ya mwanakondoo dume wa dhabihu ya ushirika yanavyoondolewa, na kuhani atayateketeza kwenye madhabahu juu ya dhabihu za Yehova zinazochomwa kwa moto;+ naye kuhani atatoa dhabihu ya kufunika dhambi ambayo mtu huyo alitenda, naye atasamehewa.+

5 “‘Ikiwa mtu amesikia mwito wa hadharani wa kutoa ushahidi*+ kuhusu jambo ambalo amejionea au kusikia au kujua, lakini amekataa kutoa habari, basi ametenda dhambi, naye atawajibika kwa sababu ya kosa lake.

2 “‘Au mtu akigusa kitu chochote kisicho safi, iwe ni mzoga wa mnyama wa mwituni, mzoga wa mnyama wa kufugwa, au viumbe wanaoishi katika makundi makubwa,+ hatakuwa safi na atakuwa na hatia hata kama hajui jambo hilo. 3 Au mtu akigusa uchafu wa mwanadamu bila kujua+—kitu chochote kisicho safi kinachoweza kumchafua—atakuwa na hatia atakapojua jambo hilo.

4 “‘Au mtu akiapa kufanya jambo fulani bila kufikiri—jambo lolote lile, jema au baya—lakini baadaye atambue kwamba ameapa bila kufikiri, atakuwa na hatia atakapojua jambo hilo.*+

5 “‘Ikiwa ana hatia katika jambo lolote kati ya mambo hayo, basi ni lazima aungame+ dhambi aliyotenda. 6 Pia atamletea Yehova dhabihu ya hatia kwa ajili ya dhambi aliyotenda;+ ataleta mnyama jike kutoka katika kundi, yaani, mwanakondoo jike au mwanambuzi jike, ili awe dhabihu ya dhambi. Kisha kuhani atamtolea dhabihu ya kufunika dhambi yake.

7 “‘Hata hivyo, ikiwa hawezi kutoa kondoo, atamletea Yehova njiwa tetere wawili au hua wawili wachanga+ wawe dhabihu ya hatia kwa ajili ya dhambi yake, ndege mmoja kwa ajili ya dhabihu ya dhambi, na mwingine kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa.+ 8 Atawaleta kwa kuhani, naye kuhani atatoa ndege mmoja kwanza kwa ajili ya dhabihu ya dhambi, atamvunja shingo na kuacha kichwa kikining’inia. 9 Atanyunyiza kiasi kidogo cha damu ya dhabihu hiyo ya dhambi kando ya madhabahu, lakini damu inayobaki itamwagwa kwenye msingi wa madhabahu.+ Ni dhabihu ya dhambi. 10 Atamtoa ndege wa pili kuwa dhabihu ya kuteketezwa akifuata utaratibu wa kawaida;+ naye kuhani atamtolea dhabihu ya kufunika dhambi aliyotenda, naye atasamehewa.+

11 “‘Ikiwa hawezi kutoa njiwa tetere wawili au hua wawili wachanga, basi atatoa sehemu ya kumi ya kipimo cha efa moja*+ ya unga laini ili kuwa dhabihu ya dhambi. Hapaswi kuutia mafuta au ubani kwa sababu ni dhabihu ya dhambi. 12 Atauleta kwa kuhani, naye kuhani atachukua mkono mmoja wa unga huo ukiwa dhabihu ya kumbukumbu* naye atauweka kwenye madhabahu juu ya dhabihu za Yehova zinazochomwa kwa moto ili ufuke moshi. Ni dhabihu ya dhambi. 13 Kuhani atamtolea dhabihu ya kufunika dhambi aliyotenda, yoyote kati ya dhambi hizo, naye atasamehewa.+ Sehemu inayobaki ya dhabihu hiyo itakuwa ya kuhani,+ sawa na sehemu inayobaki ya toleo la nafaka.’”+

14 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 15 “Mtu akikosa uaminifu kwa kutenda dhambi bila kukusudia kwa kuvunja sheria kuhusu vitu vitakatifu vya Yehova,+ anapaswa kumletea Yehova kondoo dume asiye na kasoro kutoka kundini ili awe dhabihu ya hatia;+ thamani yake itapimwa kwa shekeli za fedha* kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu.*+ 16 Naye atalipia dhambi aliyotenda dhidi ya mahali patakatifu na pia ataongeza sehemu ya tano ya thamani ya vitu hivyo.+ Atampa kuhani, ili kuhani amtolee dhabihu ya kufunika dhambi+ yake akitumia kondoo dume wa dhabihu ya hatia, naye atasamehewa.+

17 “Mtu akitenda dhambi kwa kufanya jambo lolote ambalo Yehova ameamuru lisifanywe, hata kama hajui, bado ana hatia naye atawajibika kwa sababu ya kosa lake.+ 18 Anapaswa kumletea kuhani kondoo dume asiye na kasoro kutoka kundini kulingana na thamani iliyokadiriwa, kwa ajili ya dhabihu ya hatia.+ Kisha kuhani atamtolea dhabihu ya kufunika kosa alilofanya bila kukusudia na bila kujua, naye atasamehewa. 19 Ni dhabihu ya hatia. Bila shaka ana hatia ya kumtendea dhambi Yehova.”

6 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Mtu akitenda dhambi na kukosa uaminifu kwa Yehova+ kwa kumdanganya jirani yake kuhusu kitu fulani alichokabidhiwa atunze,+ au alichoachiwa kama dhamana, au akimwibia au kumlaghai jirani yake, 3 au akipata kitu kilichopotea na kudanganya kwamba hajakipata, naye akiapa kwa uwongo kuhusu dhambi yoyote kama hiyo ambayo huenda akatenda,+ anapaswa kufanya hivi: 4 Ikiwa ametenda dhambi naye ana hatia, ni lazima arudishe kitu alichoiba, kitu alichochukua kwa nguvu, kitu alichochukua kwa ulaghai, kitu alichokabidhiwa atunze, au kitu kilichopotea akakipata, 5 au chochote alichoapia kwa uwongo, ni lazima alipe kitu hicho kikamili+ na kuongeza sehemu ya tano ya thamani yake. Atamrudishia mwenyewe kitu hicho siku ambayo hatia yake itajulikana. 6 Naye atamletea kuhani kondoo dume asiye na kasoro kutoka kundini ili amtolee Yehova dhabihu ya hatia kulingana na thamani iliyokadiriwa ya dhabihu ya hatia.+ 7 Kuhani atamtolea dhabihu ya kufunika dhambi yake mbele za Yehova, naye atasamehewa kosa lolote ambalo lilifanya awe na hatia.”+

8 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 9 “Mwamuru hivi Haruni na wanawe: ‘Hii ndiyo sheria kuhusu dhabihu ya kuteketezwa:+ Dhabihu ya kuteketezwa itakaa usiku kucha motoni juu ya madhabahu mpaka asubuhi, hakikisheni kwamba moto wa madhabahu unaendelea kuwaka. 10 Kuhani atavaa vazi lake rasmi la kitani+ na suruali fupi ya kitani.*+ Kisha ataondoa majivu*+ ya dhabihu iliyoteketezwa kwenye madhabahu na kuyaweka kando ya madhabahu. 11 Halafu atavua mavazi hayo+ na kuvaa mengine, naye atapeleka majivu hayo mahali safi nje ya kambi.+ 12 Ni lazima moto wa madhabahu uendelee kuwaka. Haupaswi kuzimika. Kila asubuhi kuhani ataongeza kuni+ kwenye moto huo na kupanga dhabihu ya kuteketezwa juu yake, naye atateketeza mafuta ya dhabihu za ushirika ili yafuke moshi.+ 13 Hakikisheni kwamba moto unaendelea kuwaka daima kwenye madhabahu. Haupaswi kuzimika.

14 “‘Hii ndiyo sheria kuhusu toleo la nafaka:+ Ninyi wana wa Haruni mtamtolea Yehova toleo hilo mbele ya madhabahu. 15 Mmoja wenu atachukua mkono mmoja wa unga laini wa toleo la nafaka na kiasi fulani cha mafuta yake na ubani wote ulio katika toleo la nafaka, naye atauteketeza ili ufuke moshi kwenye madhabahu kama harufu ya kupendeza* ya dhabihu ya kumbukumbu* kwa Yehova.+ 16 Haruni na wanawe watatumia unga unaobaki+ kuoka mikate isiyo na chachu, nao watakula mikate hiyo mahali patakatifu. Wataila katika ua wa hema la mkutano.+ 17 Haipaswi kuokwa pamoja na kitu chochote chenye chachu.+ Nimewapa liwe fungu lao kutoka katika matoleo yangu yanayochomwa kwa moto.+ Ni toleo takatifu kabisa,+ kama ilivyo dhabihu ya dhambi na dhabihu ya hatia. 18 Kila mzao wa kiume wa Haruni ataila.+ Ni posho yao ya kudumu katika vizazi vyenu vyote kutoka kwa matoleo ya Yehova yanayochomwa kwa moto.+ Chochote kinachogusa matoleo hayo kitakuwa kitakatifu.’”

19 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 20 “Hivi ndivyo vitu ambavyo Haruni na wanawe watamtolea Yehova siku ambayo Haruni atatiwa mafuta:+ sehemu ya kumi ya kipimo cha efa moja*+ ya unga laini kama toleo la kawaida la nafaka,+ nusu ya unga huo asubuhi na nusu nyingine jioni. 21 Utachanganywa na mafuta na kuokwa kwenye kiokeo.+ Mtaukanda vizuri kabisa kwa mafuta na kuuleta ukiwa vitumbua vya toleo la nafaka lenye harufu inayompendeza* Yehova. 22 Mwana wa Haruni atakayetiwa mafuta ili kuwa kuhani baada yake+ atatoa toleo hilo. Ni sheria ya kudumu: Kwa kuwa toleo hilo linatolewa kwa Yehova likiwa zima litateketezwa ili moshi ufuke mbele zake. 23 Kila toleo la nafaka la kuhani linapaswa kuwa toleo zima. Halipaswi kuliwa.”

24 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 25 “Mwambie hivi Haruni na wanawe: ‘Hii ndiyo sheria kuhusu dhabihu ya dhambi:+ Mnyama wa dhabihu ya dhambi atachinjiwa+ mahali ambapo mnyama wa dhabihu ya kuteketezwa huchinjwa mbele za Yehova. Ni dhabihu takatifu kabisa. 26 Kuhani anayetoa dhabihu hiyo kwa ajili ya dhambi ataila.+ Ataila mahali patakatifu katika ua wa hema la mkutano.+

27 “‘Kila kitu kinachogusa nyama hiyo kitakuwa kitakatifu, na vazi la mtu yeyote likidondokewa na damu ya mnyama huyo, mtalifua vazi hilo mahali patakatifu. 28 Chombo cha udongo kilichotumiwa kuchemshia nyama hiyo kitavunjwavunjwa. Lakini ikiwa ilichemshiwa katika chombo cha shaba, basi lazima chombo hicho kisuguliwe na kusafishwa kwa maji.

29 “‘Kila mwanamume kuhani ataila.+ Ni takatifu kabisa.+ 30 Lakini kila dhabihu ya dhambi ambayo kiasi fulani cha damu yake kimeletwa mahali patakatifu kwenye hema la mkutano ili kufunika dhambi, haitaliwa.+ Itateketezwa.

7 “‘Hii ndiyo sheria kuhusu dhabihu ya hatia:+ Ni dhabihu takatifu kabisa. 2 Mnyama wa dhabihu ya hatia atachinjiwa mahali ambapo dhabihu za kuteketezwa huchinjwa, na damu yake+ itanyunyizwa pande zote za madhabahu.+ 3 Kuhani atatoa mafuta yote+ ya mnyama huyo pamoja na mkia wake wenye mafuta, mafuta yanayofunika matumbo, 4 na figo zake mbili pamoja na mafuta yake yaliyo karibu na kiuno. Ataondoa pia figo pamoja na mafuta yaliyo juu ya ini.+ 5 Kuhani ataviteketeza vitu hivyo kwenye madhabahu ili vifuke moshi vikiwa dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto.+ Ni dhabihu ya hatia. 6 Kila mwanamume kuhani ataila,+ nayo inapaswa kuliwa mahali patakatifu. Ni dhabihu takatifu kabisa.+ 7 Sheria kuhusu dhabihu ya dhambi ni sawa na sheria kuhusu dhabihu ya hatia; dhabihu hiyo ni ya kuhani aliyeitoa kufunika dhambi.+

8 “‘Kuhani akitoa dhabihu ya kuteketezwa kwa ajili ya mtu, ngozi+ ya mnyama aliyeletwa kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa itakuwa ya kuhani huyo.

9 “‘Kila toleo la nafaka linalookwa kwenye jiko au kikaangio au kiokeo+ ni la kuhani anayelitoa. Litakuwa lake.+ 10 Lakini kila toleo la nafaka linalochanganywa na mafuta+ au lililo kavu+ litakuwa la wana wote wa Haruni; kila mmoja wao atapokea kiasi kilekile.

11 “‘Sasa hii ndio sheria ya dhabihu ya ushirika+ ambayo mtu yeyote anaweza kumtolea Yehova: 12 Ikiwa anaitoa ili kuonyesha shukrani,+ ataitoa dhabihu hiyo ya shukrani pamoja na mikate ya mviringo isiyo na chachu na iliyokandwa kwa mafuta, mikate myembamba isiyo na chachu na ambayo imepakwa mafuta, na mikate ya mviringo iliyookwa kwa unga laini uliochanganywa vizuri kabisa na kukandwa kwa mafuta. 13 Atatoa dhabihu yake pamoja na mikate ya mviringo iliyotiwa chachu na dhabihu ya shukrani ya dhabihu zake za ushirika. 14 Atatoa mkate mmoja kutoka katika kila toleo kuwa fungu takatifu kwa Yehova; litakuwa la kuhani anayenyunyiza damu ya dhabihu za ushirika.+ 15 Nyama za dhabihu za ushirika zinazotolewa ili kuonyesha shukrani zinapaswa kuliwa siku ambayo dhabihu hiyo ya shukrani inatolewa. Nyama yoyote ya dhabihu hiyo haipaswi kuachwa mpaka asubuhi.+

16 “‘Ikiwa dhabihu anayotoa ni kwa ajili ya nadhiri+ au ni toleo la hiari,+ inapaswa kuliwa siku ambayo anatoa dhabihu hiyo, na nyama inayobaki inaweza pia kuliwa siku inayofuata. 17 Lakini nyama yoyote inayobaki ya dhabihu hiyo inapaswa kuteketezwa siku ya tatu.+ 18 Hata hivyo, nyama yoyote ya dhabihu ya ushirika ikiliwa siku ya tatu, yule anayeitoa hatapata kibali. Haitamnufaisha; ni dhabihu inayochukiza, na mtu anayeila ataadhibiwa kwa sababu ya kosa lake.+ 19 Nyama inayogusa kitu chochote kisicho safi haipaswi kuliwa. Itateketezwa kwa moto. Mtu yeyote aliye safi anaweza kula nyama iliyo safi.

20 “‘Lakini mtu yeyote asiye safi akila nyama ya dhabihu ya ushirika, ambayo ni ya Yehova, ni lazima auawe.+ 21 Mtu yeyote akigusa kitu chochote kisicho safi, iwe ni uchafu wa mwanadamu+ au mnyama asiye safi+ au kitu chochote chenye kuchukiza kisicho safi,+ kisha ale nyama ya dhabihu ya ushirika, ambayo ni ya Yehova, ni lazima auawe.’”

22 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 23 “Waambie Waisraeli, ‘Hampaswi kula mafuta yoyote+ ya ng’ombe dume au ya mwanakondoo dume au ya mbuzi. 24 Mafuta ya mnyama aliyepatikana amekufa na mafuta ya mnyama aliyeuawa na mnyama mwingine, yanaweza kutumiwa kwa kusudi lingine lolote, lakini hampaswi kamwe kuyala.+ 25 Kwa maana mtu yeyote anayekula mafuta ya mnyama anayemtoa kuwa dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto, ni lazima auawe.

26 “‘Hampaswi kula damu yoyote+ mahali popote mnapoishi, iwe ni damu ya ndege au ya mnyama. 27 Mtu yeyote anayekula damu ni lazima auawe.’”+

28 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 29 “Waambie Waisraeli, ‘Mtu yeyote anayemletea Yehova dhabihu yake ya ushirika atamtolea Yehova sehemu ya dhabihu hiyo.+ 30 Ataleta mafuta+ pamoja na kidari kwa mikono yake mwenyewe ili vitu hivyo viwe dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto, naye atavitikisa kwenda mbele na nyuma vikiwa toleo la kutikiswa+ mbele za Yehova. 31 Kuhani atayateketeza mafuta hayo kwenye madhabahu ili yafuke moshi,+ lakini kidari kitakuwa cha Haruni na wanawe.+

32 “‘Mtampa kuhani mguu wa kulia kutoka katika dhabihu zenu za ushirika ukiwa fungu takatifu.+ 33 Mguu wa kulia utakuwa fungu la mwana wa Haruni atakayetoa damu ya dhabihu za ushirika na mafuta.+ 34 Kwa maana nachukua kidari cha toleo la kutikiswa na mguu wa lile fungu takatifu kutoka kwa dhabihu za ushirika za Waisraeli na kumpa kuhani Haruni na wanawe. Ni sheria ya kudumu kwa Waisraeli.+

35 “‘Hilo ndilo fungu lililotengwa kwa ajili ya makuhani, yaani, Haruni na wanawe, kutoka katika dhabihu za Yehova zinazochomwa kwa moto, fungu lililotengwa kwa ajili yao siku waliyowekwa rasmi kumtumikia Yehova wakiwa makuhani.+ 36 Yehova aliwaamuru Waisraeli wawape makuhani fungu hilo siku alipowatia mafuta.+ Ni sheria ya kudumu katika vizazi vyao.’”

37 Hizo ndizo sheria kuhusu dhabihu ya kuteketezwa,+ toleo la nafaka,+ dhabihu ya dhambi,+ dhabihu ya hatia,+ dhabihu ya kuwaweka rasmi makuhani,+ na dhabihu ya ushirika,+ 38 kama Yehova alivyomwamuru Musa kwenye Mlima Sinai+ siku aliyowaamuru Waisraeli wamtolee Yehova dhabihu zao katika nyika ya Sinai.+

8 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Mchukue Haruni na wanawe,+ pamoja na mavazi yao,+ na mafuta yanayotumiwa kutia mafuta,+ ng’ombe dume wa dhabihu ya dhambi, kondoo dume wawili, na kikapu cha mikate isiyo na chachu,+ 3 uwakusanye Waisraeli wote kwenye mlango wa hema la mkutano.”

4 Basi Musa akafanya kama Yehova alivyomwamuru, Waisraeli wote wakakusanyika kwenye mlango wa hema la mkutano. 5 Musa akawaambia: “Hili ndilo jambo ambalo Yehova ameamuru tufanye.” 6 Kwa hiyo Musa akamleta Haruni na wanawe na kuwaosha kwa maji.+ 7 Kisha akamvisha kanzu,+ akamfunga ukumbuu,+ akamvisha lile joho lisilo na mikono,+ akamvisha efodi+ na kumfunga vizuri kabisa mshipi wa efodi uliofumwa.+ 8 Halafu akamvisha kifuko cha kifuani+ na kutia Urimu na Thumimu+ ndani ya kifuko hicho. 9 Kisha akamvisha kilemba+ kichwani na kuweka lile bamba linalong’aa la dhahabu upande wa mbele wa kilemba hicho, ile ishara takatifu ya wakfu,*+ kama Yehova alivyomwamuru Musa.

10 Kisha Musa akachukua mafuta yanayotumiwa kutia mafuta akalitia mafuta hema la ibada na vitu vyote vilivyokuwa ndani yake,+ akavitakasa. 11 Baada ya hayo akanyunyiza kiasi fulani cha mafuta hayo juu ya madhabahu mara saba na kuitia mafuta madhabahu, vyombo vyake vyote, na pia beseni na kinara chake, ili kuvitakasa. 12 Mwishowe akamimina juu ya kichwa cha Haruni kiasi fulani cha mafuta hayo yanayotumiwa kutia mafuta, akamtia mafuta ili kumtakasa.+

13 Halafu Musa akawaleta wana wa Haruni, akawavisha kanzu, akawafunga ukumbuu, na kuwavisha kofia,+ kama Yehova alivyomwamuru Musa.

14 Kisha akamleta ng’ombe dume wa dhabihu ya dhambi, Haruni na wanawe wakaweka mikono yao juu ya kichwa cha ng’ombe dume huyo wa dhabihu ya dhambi.+ 15 Musa akamchinja, akachukua damu yake+ kwa kidole chake na kuzipaka pembe zote za madhabahu, akaitakasa madhabahu kutokana na dhambi, lakini damu iliyobaki aliimwaga kwenye msingi wa madhabahu, ili aitakase na kutoa juu yake dhabihu ya kufunika dhambi. 16 Kisha Musa akachukua mafuta yote yaliyofunika matumbo, mafuta yaliyo juu ya ini, na figo mbili pamoja na mafuta yake, akateketeza vitu hivyo juu ya madhabahu ili vifuke moshi.+ 17 Kisha akachukua sehemu zilizobaki za ng’ombe dume huyo, ngozi yake, nyama yake, na mavi yake, akateketeza sehemu hizo nje ya kambi,+ kama Yehova alivyomwamuru Musa.

18 Halafu akamleta kondoo dume wa dhabihu ya kuteketezwa, Haruni na wanawe wakaweka mikono yao juu ya kichwa cha kondoo dume huyo.+ 19 Musa akamchinja na kunyunyiza damu yake pande zote za madhabahu. 20 Akamkata kondoo huyo vipandevipande, akateketeza kichwa, vipande alivyokata, na mafuta yaliyo kwenye figo, ili vifuke moshi. 21 Akaosha matumbo na miguu kwa maji na kumteketeza kondoo dume mzima kwenye madhabahu ili afuke moshi. Ilikuwa dhabihu ya kuteketezwa yenye harufu inayopendeza.* Ilikuwa dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto, kama Yehova alivyomwamuru Musa.

22 Kisha akamleta kondoo dume wa pili, kondoo wa kuwaweka rasmi makuhani,+ basi Haruni na wanawe wakaweka mikono yao juu ya kichwa cha kondoo huyo.+ 23 Musa akamchinja na kuchukua kiasi fulani cha damu yake na kuipaka kwenye ncha ya sikio la kulia la Haruni na kwenye kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kwenye kidole gumba cha mguu wake wa kulia. 24 Kisha Musa akawaleta wana wa Haruni na kuwapaka damu hiyo kwenye ncha za masikio yao ya kulia na kwenye vidole gumba vya mikono yao ya kulia na kwenye vidole gumba vya miguu yao ya kulia; lakini damu iliyobaki Musa aliinyunyiza pande zote za madhabahu.+

25 Kisha akachukua yale mafuta, mkia wenye mafuta, mafuta yote yaliyofunika matumbo, mafuta yote yaliyokuwa juu ya ini, zile figo mbili na mafuta yake, na mguu wa kulia.+ 26 Akachukua mkate mmoja wa mviringo usio na chachu,+ mkate mmoja wa mviringo wenye mafuta,+ na mkate mmoja mwembamba kutoka katika kikapu cha mikate isiyo na chachu kilichokuwa mbele za Yehova. Akaiweka mikate hiyo juu ya vipande vya mafuta na juu ya mguu wa kulia. 27 Baada ya hayo akaviweka vitu hivyo vyote katika mikono ya Haruni na mikono ya wanawe na kuanza kuvitikisa kwenda mbele na nyuma vikiwa toleo la kutikiswa mbele za Yehova. 28 Kisha Musa akavichukua kutoka mikononi mwao na kuviteketeza kwenye madhabahu juu ya dhabihu ya kuteketezwa ili vifuke moshi. Vitu hivyo vilikuwa dhabihu ya kuwaweka rasmi makuhani, dhabihu yenye harufu ya kupendeza.* Vilikuwa dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto.

29 Kisha Musa akachukua kidari na kukitikisa kwenda mbele na nyuma kikiwa toleo la kutikiswa mbele za Yehova.+ Sehemu hiyo ya kondoo wa kuwaweka rasmi makuhani ilikuwa fungu la Musa, kama Yehova alivyomwamuru Musa.+

30 Halafu Musa akachukua kiasi kidogo cha mafuta yanayotumiwa kutia mafuta+ na kiasi kidogo cha damu iliyokuwa kwenye madhabahu, akamnyunyizia Haruni na mavazi yake na pia wanawe na mavazi yao. Basi akamtakasa Haruni na mavazi yake na pia wanawe+ na mavazi yao.+

31 Kisha Musa akamwambia Haruni na wanawe: “Chemsheni+ nyama hiyo kwenye mlango wa hema la mkutano, na muile hapo mlangoni pamoja na mikate iliyo katika kikapu cha kuwaweka rasmi makuhani, kama nilivyoamriwa kwamba, ‘Haruni na wanawe wataila.’+ 32 Mtateketeza nyama na mikate itakayobaki.+ 33 Hampaswi kutoka nje ya mlango wa hema la mkutano kwa siku saba, mpaka siku zenu za kuwekwa rasmi kuwa makuhani zitakapokwisha, kwa sababu itachukua muda wa siku saba kuwaweka rasmi kuwa makuhani.+ 34 Yehova alituamuru tufanye mambo tuliyofanya leo ili tuwatolee dhabihu ya kufunika dhambi zenu.+ 35 Mtakaa kwenye mlango wa hema la mkutano kwa siku saba,+ mchana na usiku, nanyi mtatimiza wajibu wenu mbele za Yehova,+ msije mkafa; hivyo ndivyo nilivyoamriwa.”

36 Basi Haruni na wanawe wakafanya mambo yote ambayo Yehova aliamuru kupitia Musa.

9 Siku ya nane,+ Musa akamwita Haruni na wanawe na wazee wa Israeli. 2 Akamwambia Haruni: “Chukua ndama mchanga kwa ajili ya dhabihu ya dhambi+ na kondoo dume kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa, wanyama wasio na kasoro, nawe uwatoe mbele za Yehova. 3 Lakini utawaambia Waisraeli ‘Chukueni mbuzi dume kwa ajili ya dhabihu ya dhambi na ndama na mwanakondoo dume, wote wa umri wa mwaka mmoja na wasio na kasoro, kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa, 4 na ng’ombe dume na kondoo dume kwa ajili ya dhabihu za ushirika,+ ili muwatoe dhabihu mbele za Yehova, na pia toleo la nafaka+ lililochanganywa na mafuta, kwa sababu leo Yehova atawatokea.’”+

5 Basi wakapeleka vitu ambavyo Musa aliamuru mbele ya hema la mkutano. Halafu Waisraeli wote wakaja na kusimama mbele za Yehova. 6 Musa akasema: “Hili ndilo jambo ambalo Yehova amewaamuru mfanye, ili muone utukufu wa Yehova.”+ 7 Kisha Musa akamwambia Haruni: “Nenda kwenye madhabahu, utoe dhabihu yako ya dhambi+ na dhabihu yako ya kuteketezwa, utoe dhabihu ya kufunika dhambi zako mwenyewe+ na za nyumba yako; kisha uwatolee watu dhabihu ya kufunika dhambi zao,+ kama Yehova alivyoamuru.”

8 Haruni akaenda mara moja kwenye madhabahu na kumchinja yule ndama wa dhabihu ya dhambi kwa ajili yake mwenyewe.+ 9 Kisha wanawe wakamletea damu,+ naye akachovya kidole chake katika damu hiyo na kupaka pembe za madhabahu, na damu iliyobaki akaimwaga kwenye msingi wa madhabahu.+ 10 Akateketeza mafuta na figo na mafuta yaliyo juu ya ini kutoka katika dhabihu ya dhambi ili vifuke moshi kwenye madhabahu, kama Yehova alivyomwamuru Musa.+ 11 Naye akateketeza nyama na ngozi nje ya kambi.+

12 Kisha Haruni akamchinja mnyama wa dhabihu ya kuteketezwa na wanawe wakampa damu, naye akainyunyiza pande zote za madhabahu.+ 13 Wakampa vipande vya mnyama wa dhabihu ya kuteketezwa pamoja na kichwa, naye akaviteketeza ili vifuke moshi kwenye madhabahu. 14 Pia, akaosha matumbo na miguu, akaviteketeza vitu hivyo kwenye madhabahu juu ya dhabihu ya kuteketezwa ili vifuke moshi.

15 Kisha akatoa dhabihu kwa ajili ya watu; akamchukua yule mbuzi wa dhabihu ya dhambi aliyepaswa kutolewa kwa ajili ya watu, akamchinja na kutoa dhabihu ya dhambi kama alivyofanya kwa yule wa kwanza. 16 Akatoa dhabihu ya kuteketezwa akifuata utaratibu wa kawaida.+

17 Kisha akatoa toleo la nafaka;+ akachukua mkono mmoja wa toleo hilo na kuliteketeza ili lifuke moshi kwenye madhabahu pamoja na dhabihu ya kuteketezwa ya asubuhi.+

18 Baada ya hayo Haruni akamchinja yule ng’ombe dume na kondoo dume wa dhabihu ya ushirika aliyepaswa kutolewa kwa ajili ya watu. Kisha wanawe wakampa damu, akainyunyiza pande zote za madhabahu.+ 19 Lakini vipande vyenye mafuta vya ng’ombe dume,+ mkia wenye mafuta wa kondoo dume, mafuta yaliyofunika matumbo, na figo, na mafuta yaliyokuwa juu ya ini,+ 20 waliviweka vipande hivyo vyote vyenye mafuta juu ya vidari, kisha akaviteketeza vipande hivyo ili vifuke moshi kwenye madhabahu.+ 21 Hata hivyo, Haruni akatikisa vidari na mguu wa kulia kwenda mbele na nyuma kuwa toleo la kutikiswa mbele za Yehova, kama Musa alivyoamuru.+

22 Kisha Haruni akainua mikono yake kuelekea watu, akawabariki,+ naye akashuka chini baada ya kutoa dhabihu ya dhambi na dhabihu ya kuteketezwa na dhabihu za ushirika. 23 Mwishowe Musa na Haruni wakaingia katika hema la mkutano, kisha wakatoka nje na kuwabariki watu.+

Ndipo watu wote wakauona utukufu wa Yehova,+ 24 na moto ukashuka kutoka kwa Yehova+ na kuanza kuteketeza ile dhabihu ya kuteketezwa na vile vipande vyenye mafuta vilivyokuwa kwenye madhabahu. Watu wote walipoona hilo, wakaanza kupaza sauti na kuanguka kifudifudi.+

10 Baadaye Nadabu na Abihu,+ wana wa Haruni, walichukua kila mmoja wao chetezo chake, wakaweka moto ndani yake na kutia uvumba.+ Wakaanza kumtolea Yehova moto haramu,+ jambo ambalo hakuwaamuru wafanye. 2 Ndipo moto ukashuka kutoka kwa Yehova, ukawateketeza,+ wakafa mbele za Yehova.+ 3 Musa akamwambia Haruni: “Yehova amesema hivi: ‘Nitatakaswa miongoni mwa wale walio karibu nami,+ nami nitatukuzwa mbele ya watu wote.’” Haruni akanyamaza kimya.

4 Basi Musa akamwita Mishaeli na Elsafani, wana wa Uzieli,+ ndugu ya baba ya Haruni, akawaambia: “Njooni hapa, waondoeni ndugu zenu mbele ya mahali patakatifu muwapeleke nje ya kambi.” 5 Kwa hiyo wakaja, wakawabeba wakiwa na kanzu zao na kuwapeleka nje ya kambi, kama Musa alivyowaambia.

6 Kisha Musa akamwambia Haruni na wanawe waliobaki, Eleazari na Ithamari: “Msikose kutunza nywele zenu na msirarue mavazi yenu,+ msije mkafa na kumfanya Mungu awakasirikie Waisraeli wote. Ndugu zenu wote wa nyumba ya Israeli watawaombolezea wale ambao Yehova amewaangamiza kwa moto. 7 Msitoke nje ya mlango wa hema la mkutano msije mkafa, kwa sababu Yehova amewatia mafuta.”+ Basi wakafanya kama Musa alivyosema.

8 Kisha Yehova akamwambia Haruni: 9 “Wewe na wanao msinywe divai au kileo chochote mnapoingia katika hema la mkutano,+ msije mkafa. Ni sheria ya kudumu katika vizazi vyenu. 10 Ili muweze kutofautisha mambo matakatifu na mambo yaliyo najisi, mambo safi na mambo yasiyo safi,+ 11 na ili muwafundishe Waisraeli wote sheria zote ambazo* Yehova amewaambia kupitia Musa.”+

12 Kisha Musa akamwambia Haruni na wanawe waliobaki, Eleazari na Ithamari: “Chukueni toleo la nafaka lililobaki kutoka katika dhabihu za Yehova zinazochomwa kwa moto, mle toleo hilo karibu na madhabahu kama mkate usio na chachu,+ kwa sababu ni toleo takatifu kabisa.+ 13 Mtakula toleo hilo mahali patakatifu,+ kwa sababu ni posho yenu na posho ya wana wenu kutoka kwenye dhabihu za Yehova zinazochomwa kwa moto, kwa maana hivyo ndivyo nilivyoamriwa. 14 Pia, wewe na wanao na binti zako+ mtakula kidari cha toleo la kutikiswa na mguu wa fungu takatifu+ mkiwa mahali safi kwa sababu vitu hivyo vimetolewa ili kuwa posho yako na posho ya wanao kutoka kwenye dhabihu za ushirika za Waisraeli. 15 Watauleta mguu wa fungu takatifu na kidari cha toleo la kutikiswa pamoja na dhabihu za mafuta zinazochomwa kwa moto, ili vitikiswe mbele za Yehova vikiwa toleo la kutikiswa kwenda mbele na nyuma; hilo litakuwa posho yako na posho ya kudumu ya wanao,+ kama Yehova alivyoamuru.”

16 Musa akamtafuta sana mbuzi wa dhabihu ya dhambi,+ lakini akagundua kwamba alikuwa ameteketezwa. Kwa hiyo akawakasirikia sana Eleazari na Ithamari, wana waliobaki wa Haruni, akawauliza: 17 “Kwa nini hamkula dhabihu ya dhambi mkiwa mahali patakatifu,+ wakati ni dhabihu takatifu kabisa ambayo amewapa ili mbebe dhambi za Waisraeli wote na kuwatolea dhabihu ya kufunika dhambi zao mbele za Yehova? 18 Sasa angalieni! Damu yake haijaletwa mahali patakatifu.+ Mlipaswa kula dhabihu hiyo mahali patakatifu, kama nilivyoamriwa.” 19 Haruni akamjibu Musa: “Tazama! Leo walimtolea Yehova dhabihu yao ya dhambi na dhabihu yao ya kuteketezwa,+ na bado mambo haya yamenipata. Kama ningekula dhabihu ya dhambi leo, je, jambo hilo lingempendeza Yehova?” 20 Musa aliposikia hayo, akaridhika.

11 Kisha Yehova akawaambia Musa na Haruni: 2 “Waambieni Waisraeli, ‘Hawa ndio wanyama wa nchi kavu mnaoweza kula:+ 3 Mnaweza kumla kila mnyama mwenye kwato zilizopasuka na zilizogawanyika anayecheua.

4 “‘Lakini hampaswi kuwala wanyama wafuatao wanaocheua au wenye kwato zilizogawanyika: msimle ngamia kwa sababu anacheua lakini kwato zake hazijagawanyika. Yeye si safi kwenu.+ 5 Pia, msimle wibari+ kwa sababu anacheua lakini kwato zake hazijagawanyika. Yeye si safi kwenu. 6 Pia, msimle sungura kwa sababu anacheua lakini kwato zake hazijagawanyika. Yeye si safi kwenu. 7 Pia, msimle nguruwe+ kwa sababu ana kwato zilizopasuka na kugawanyika lakini hacheui. Yeye si safi kwenu. 8 Msile kamwe nyama yao wala kugusa mizoga yao. Hao si safi kwenu.+

9 “‘Kati ya viumbe wote wanaoishi ndani ya maji, mnaweza kula wafuatao: Mnaweza kumla kiumbe yeyote wa majini mwenye mapezi na magamba anayeishi baharini au mtoni.+ 10 Lakini kiumbe yeyote anayeishi baharini na mtoni ambaye hana mapezi na magamba, kati ya viumbe wote wa majini wanaoishi katika makundi makubwa na viumbe wengine wote wanaoishi majini, ni chukizo kwenu. 11 Naam, watakuwa chukizo kwenu, msile kamwe nyama yao,+ nanyi mnapaswa kuchukia mizoga yao. 12 Kiumbe yeyote wa majini ambaye hana mapezi na magamba ni chukizo kwenu.

13 “‘Hawa ndio ndege mnaopaswa kuchukia; wasiliwe kwa sababu ni chukizo: tai,+ furukombe, tumbusi* mweusi,+ 14 mwewe mwekundu na aina zote za mwewe weusi, 15 kila aina ya kunguru, 16 mbuni, bundi, shakwe, kila aina ya kipanga, 17 bundi mdogo, mnandi, bundi mwenye masikio marefu, 18 batamaji, mwari, tumbusi,* 19 korongo, kila aina ya kulastara, hudihudi, na popo. 20 Kila kiumbe mwenye mabawa* anayeishi katika makundi makubwa anayetambaa kwa miguu yote minne ni chukizo kwenu.

21 “‘Kati ya wadudu wote wenye mabawa wanaoishi katika makundi makubwa na wanaotambaa kwa miguu yote minne, mnaweza kula tu wadudu wenye vifundo miguuni wanaoruka ardhini. 22 Hawa ndio mnaoweza kula: kila aina ya nzige wanaohama, nzige wengine wanaoliwa,+ chenene,* na panzi. 23 Wadudu wengine wote wenye mabawa wanaoishi katika makundi makubwa wenye miguu minne ni chukizo kwenu. 24 Wadudu hao watawafanya msiwe safi. Kila mtu anayegusa mizoga yao hatakuwa safi mpaka jioni.+ 25 Kila mtu anayebeba mizoga yao anapaswa kufua mavazi yake;+ hatakuwa safi mpaka jioni.

26 “‘Mnyama yeyote mwenye kwato zilizopasuka lakini hazijagawanyika na ambaye hacheui si safi kwenu. Kila mtu anayewagusa wanyama hao hatakuwa safi.+ 27 Kila kiumbe anayetembea kwa miguu yenye makucha kati ya viumbe wanaotembea kwa miguu minne si safi kwenu. Kila mtu anayegusa mizoga yao hatakuwa safi mpaka jioni. 28 Yeyote atakayebeba mizoga yao anapaswa kufua mavazi yake,+ hatakuwa safi mpaka jioni.+ Hao si safi kwenu.

29 “‘Hawa ndio viumbe wanaotambaa ambao si safi kwenu: fuko, panya,+ kila aina ya mjusi, 30 mjusi kafiri, mjusi mkubwa, mjusi wa majini, mjusi wa mchangani, na kinyonga. 31 Viumbe hao wanaotambaa si safi kwenu.+ Kila mtu anayegusa mizoga yao hatakuwa safi mpaka jioni.+

32 “‘Viumbe hao wakifa na kuangukia kitu chochote, kitu hicho hakitakuwa safi, iwe ni chombo cha mbao, nguo, ngozi, au gunia. Chombo chochote kinachotumiwa kinapaswa kutumbukizwa majini, nacho hakitakuwa safi mpaka jioni; baada ya hapo kitakuwa safi. 33 Wakianguka ndani ya chombo cha udongo, mnapaswa kukivunja, na chochote kilichokuwa ndani ya chombo hicho si safi.+ 34 Chakula chochote kinachomwagikiwa na maji kutoka katika chombo hicho si safi, na kinywaji chochote kutoka katika chombo hicho si safi. 35 Kitu chochote kinachoangukiwa na mizoga yao si safi. Vitu hivyo vitavunjwavunjwa iwe ni jiko kubwa au dogo. Vitu hivyo si safi, navyo havitakuwa safi kwenu. 36 Hata hivyo, chemchemi au tangi la maji litabaki safi, lakini mtu yeyote anayegusa mizoga yao hatakuwa safi. 37 Mizoga yao ikiangukia mbegu za kupandwa, zitabaki safi. 38 Lakini mbegu zikitiwa maji kisha sehemu yoyote ya mizoga yao iangukie mbegu hizo, mbegu hizo si safi kwenu.

39 “‘Mnyama yeyote mnayeruhusiwa kula akifa, yeyote anayegusa mzoga wake hatakuwa safi mpaka jioni.+ 40 Yeyote anayekula sehemu yoyote ya mzoga huo anapaswa kufua mavazi yake, hatakuwa safi mpaka jioni.+ Na yeyote anayebeba mzoga huo anapaswa kufua mavazi yake, naye hatakuwa safi mpaka jioni. 41 Kila kiumbe anayetambaa ni chukizo.+ Hapaswi kuliwa. 42 Hampaswi kumla kiumbe yeyote anayetambaa kwa tumbo, kiumbe yeyote anayetembea kwa miguu yote minne, au viumbe wowote wanaoishi katika makundi makubwa wenye miguu mingi, kwa sababu viumbe hao ni chukizo.+ 43 Msinifanye niwachukie kwa kula kiumbe yeyote kati ya viumbe hao, msijitie unajisi na kuwa watu wasio safi.+ 44 Kwa maana mimi ni Yehova Mungu wenu,+ nanyi lazima mjitakase na kuwa watakatifu,+ kwa sababu mimi ni mtakatifu.+ Kwa hiyo msijichafue kwa kula kiumbe yeyote anayetambaa. 45 Kwa maana mimi ni Yehova, ninayewaongoza kupanda kutoka nchini Misri ili nijithibitishe mwenyewe kuwa Mungu wenu,+ nanyi lazima muwe watakatifu,+ kwa sababu mimi ni mtakatifu.+

46 “‘Hiyo ndiyo sheria kuhusu wanyama, ndege, kila kiumbe anayeishi majini, na kila kiumbe anayetambaa, 47 ili kutofautisha viumbe walio safi na wasio safi na viumbe wanaoweza kuliwa na wasioweza kuliwa.’”+

12 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Waambie Waisraeli, ‘Mwanamke akipata mimba na kuzaa mtoto wa kiume, mwanamke huyo hatakuwa safi kwa siku saba, atakuwa kama anavyokuwa katika siku zake za hedhi.+ 3 Siku ya nane, mtoto huyo atatahiriwa.+ 4 Kisha kwa siku 33 mwanamke huyo ataendelea kujitakasa kwa sababu ya damu aliyopoteza. Asiguse kitu chochote kitakatifu, wala asiingie mahali patakatifu mpaka atakapokamilisha siku zake za kujitakasa.

5 “Akizaa mtoto wa kike, mwanamke huyo hatakuwa safi kwa siku 14, atakuwa kama anavyokuwa katika siku zake za hedhi. Kisha ataendelea kujitakasa kwa siku 66 kwa sababu ya damu aliyopoteza. 6 Siku zake za kujitakasa zitakapokwisha baada ya kuzaa mtoto wa kiume au wa kike, atamletea kuhani mwanakondoo dume wa mwaka mmoja kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa+ na hua mchanga au njiwa tetere kwa ajili ya dhabihu ya dhambi kwenye mlango wa hema la mkutano. 7 Kuhani atatoa dhabihu hizo mbele za Yehova ili kufunika dhambi ya mwanamke huyo, kisha atakuwa safi kutokana na damu yake. Hiyo ndiyo sheria kuhusu mwanamke anayezaa mtoto wa kiume au wa kike. 8 Lakini ikiwa hawezi kuleta kondoo, basi anapaswa kuleta njiwa tetere wawili au hua wawili wachanga,+ mmoja kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa na wa pili kwa ajili ya dhabihu ya dhambi, naye kuhani atamtolea dhabihu hizo ili kufunika dhambi yake, kisha atakuwa safi.’”

13 Yehova akaendelea kuwaambia Musa na Haruni: 2 “Ikiwa mtu ana uvimbe kwenye ngozi yake, au upele, au kigaga, au doa ambalo linaweza kuwa ugonjwa wa ukoma,*+ anapaswa kupelekwa kwa kuhani Haruni au kwa mmoja wa wanawe, makuhani.+ 3 Kuhani atachunguza sehemu iliyoathiriwa ya ngozi. Ikiwa nywele za sehemu hiyo zimebadilika kuwa nyeupe na ugonjwa umepenya chini ya ngozi, huo ni ugonjwa wa ukoma. Kuhani atauchunguza na kutangaza kwamba mtu huyo si safi. 4 Lakini ikiwa ana doa jeupe kwenye ngozi na inaonekana halijapenya chini ya ngozi na nywele hazijabadilika kuwa nyeupe, basi kuhani atamtenga mtu huyo kwa siku saba.+ 5 Kisha kuhani atamchunguza siku ya saba, na ugonjwa huo ukionekana kwamba hauendelei, nao haujaenea kwenye ngozi, atamtenga kwa siku nyingine saba.

6 “Kuhani anapaswa kumchunguza tena siku ya saba, na ikiwa ugonjwa huo umefifia na haujaenea katika ngozi, kuhani atatangaza kwamba mtu huyo ni safi;+ kilikuwa kigaga tu. Kisha mtu huyo atafua mavazi yake na kuwa safi. 7 Lakini ikiwa ni wazi kwamba kigaga hicho kimeenea* kwenye ngozi baada ya mtu huyo kwenda kwa kuhani kuthibitisha utakaso wake, basi atafika tena* mbele ya kuhani. 8 Kuhani atachunguza kigaga hicho, na ikiwa kimeenea kwenye ngozi, atatangaza kwamba mtu huyo si safi. Huo ni ukoma.+

9 “Mtu akishikwa na ukoma, ni lazima apelekwe kwa kuhani, 10 kisha kuhani atamchunguza.+ Ikiwa ana uvimbe mweupe kwenye ngozi na nywele za sehemu hiyo zimebadilika kuwa nyeupe na uvimbe huo umebadilika kuwa kidonda kibichi,+ 11 huo ni ukoma wa muda mrefu, kuhani atatangaza kwamba mtu huyo si safi. Hapaswi kumtenga,*+ kwa kuwa si safi. 12 Lakini ikiwa ukoma umeenea kwenye ngozi yote na kufunika mwili mzima kuanzia kichwani mpaka miguuni, kwa kadiri ambayo kuhani anaona, 13 na kuhani amemchunguza na kuona kwamba ukoma umefunika ngozi yake yote, atatangaza kwamba mtu huyo ni safi.* Ngozi yote imekuwa nyeupe, yeye ni safi. 14 Lakini akipata kidonda kibichi, hatakuwa safi. 15 Kuhani akikiona kidonda hicho kibichi, atatangaza kwamba mtu huyo si safi.+ Kidonda hicho kibichi si safi. Ni ukoma.+ 16 Lakini kidonda hicho kikibadilika tena na kuwa cheupe, mtu huyo ataenda kwa kuhani. 17 Kuhani atamchunguza,+ na ikiwa kimebadilika kuwa cheupe, kuhani atamtangaza kuwa safi mtu huyo aliyeambukizwa.

18 “Mtu akishikwa na jipu kisha lipone, 19 na uvimbe mweupe au doa lenye mchanganyiko wa rangi nyekundu na nyeupe litokee mahali palipokuwa na jipu hilo, ni lazima aende kwa kuhani. 20 Kuhani atachunguza doa hilo,+ na akiona kwamba limepenya chini ya ngozi na nywele za sehemu hiyo zimebadilika kuwa nyeupe, atatangaza kwamba mtu huyo si safi. Ni ugonjwa wa ukoma uliotokea mahali palipokuwa na jipu. 21 Lakini kuhani akichunguza na kuona kwamba hakuna nywele nyeupe sehemu hiyo na doa halijapenya chini ya ngozi, nalo limeanza kupona, atamtenga kwa siku saba.+ 22 Na ikiwa limeenea kwenye ngozi, kuhani atatangaza kwamba mtu huyo si safi. Ni ugonjwa. 23 Lakini doa hilo likibaki palepale na halijaenea, ni uvimbe tu wa jipu, kuhani atamtangaza kuwa safi.+

24 “Au ikiwa mtu ana kovu lililosababishwa na moto na kovu hilo bichi likigeuka rangi na kuwa doa lenye mchanganyiko wa rangi nyekundu na nyeupe au nyeupe tu, 25 kuhani atalichunguza doa hilo. Ikiwa nywele zimebadilika na kuwa nyeupe katika doa hilo na inaonekana limepenya chini ya ngozi, ni ukoma uliotokea kwenye kovu, basi kuhani atatangaza kwamba mtu huyo si safi. Ni ugonjwa wa ukoma. 26 Lakini kuhani akichunguza doa hilo na kuona halina nywele nyeupe, halijapenya chini ya ngozi, na limeanza kupona, atamtenga mtu huyo kwa siku saba.+ 27 Kuhani atamchunguza siku ya saba, na ikiwa limeenea kwenye ngozi, atatangaza kwamba mtu huyo si safi. Ni ugonjwa wa ukoma. 28 Lakini doa hilo likibaki vilevile na lisipoenea kwenye ngozi, na ikiwa limeanza kupona, ni uvimbe tu wa lile kovu, kuhani atatangaza kwamba mtu huyo ni safi, kwa sababu ni mwasho wa kovu hilo.

29 “Mwanamume au mwanamke akipata kidonda kichwani au kwenye kidevu, 30 kuhani atachunguza kidonda hicho.+ Akiona kwamba kimepenya chini ya ngozi na nywele za sehemu hiyo ni za manjano na ni chache, kuhani atatangaza kwamba mtu huyo si safi; ni ugonjwa unaoathiri ngozi ya kichwa au kidevu. Ni ukoma wa kichwa au wa kidevu. 31 Lakini kuhani akiona kwamba kidonda hicho hakijapenya chini ya ngozi na sehemu hiyo haina nywele nyeusi, anapaswa kumtenga mtu huyo kwa siku saba.+ 32 Kuhani atachunguza kidonda hicho siku ya saba, ikiwa hakijaenea au hakina nywele za manjano na hakijapenya chini ya ngozi, 33 mtu huyo anapaswa kunyolewa, lakini hatanyolewa sehemu yenye kidonda. Kisha kuhani atamtenga mtu huyo kwa siku saba.

34 “Kuhani atakichunguza tena kidonda hicho siku ya saba, na ikiwa kidonda hicho kilicho kichwani na kwenye kidevu hakijaenea au kupenya chini ya ngozi, kuhani anapaswa kutangaza kwamba mtu huyo ni safi, atafua mavazi yake na kuwa safi. 35 Lakini ikiwa kidonda kimeenea kwenye ngozi baada ya mtu huyo kutangazwa kuwa safi, 36 kuhani atamchunguza, ikiwa kidonda hicho kimeenea kwenye ngozi, kuhani hahitaji kuchunguza ikiwa kuna nywele za manjano; mtu huyo si safi. 37 Lakini akimchunguza na kuona kwamba hakijaenea na nywele nyeusi zimeota sehemu iliyokuwa na kidonda, mtu huyo amepona. Yeye ni safi, kuhani atamtangaza kuwa safi.+

38 “Mwanamume au mwanamke akiwa na madoa meupe kwenye ngozi, 39 kuhani atayachunguza.+ Ikiwa madoa hayo si meupe sana, ni vipele visivyo na madhara vilivyotokea kwenye ngozi. Mtu huyo ni safi.

40 “Ikiwa mwanamume atapata upara kichwani, yeye ni safi. 41 Akipata upara sehemu ya mbele ya kichwa, yeye ni safi. 42 Lakini mtu akipata kidonda chenye mchanganyiko wa rangi nyekundu na nyeupe kwenye upara au paji la uso, ni ukoma unaotokea kwenye upara au paji lake la uso. 43 Kuhani atamchunguza, na ikiwa kidonda kilicho kwenye upara au paji lake la uso kina uvimbe wenye mchanganyiko wa rangi nyekundu na nyeupe, na ngozi yake inaonekana ni kama ina ukoma, 44 mtu huyo ana ukoma. Yeye si safi, kuhani anapaswa kutangaza kwamba mtu huyo si safi kwa sababu ya ugonjwa aliopata kichwani. 45 Mtu mwenye ukoma anapaswa kuvaa mavazi yaliyoraruka, hapaswi kutunza nywele za kichwa chake, naye anapaswa kufunika masharubu yake na kusema hivi kwa sauti: ‘Mimi si safi, mimi si safi!’ 46 Kwa muda wote atakaokuwa na ugonjwa huo hatakuwa safi. Kwa kuwa yeye si safi, ataishi akiwa ametengwa. Ataishi nje ya kambi.+

47 “Vazi likiathiriwa na ugonjwa wa ukoma, iwe ni vazi la sufu au la kitani, 48 iwe ni ndani ya mtande au ndani ya mshindio wa kitani au wa sufu, au ndani ya ngozi au ndani ya chochote kilichotengenezwa kwa ngozi, 49 na ikiwa vazi, ngozi, mtande, mshindio, au kitu chochote cha ngozi kina doa lenye mchanganyiko wa rangi ya manjano na kijani au doa jekundu, huo ni ugonjwa wa ukoma, kuhani anapaswa kuonyeshwa vazi hilo. 50 Kuhani atachunguza ugonjwa huo, naye anapaswa kulitenga vazi hilo lenye ugonjwa kwa siku saba.+ 51 Atakapolichunguza siku ya saba na kuona kwamba ugonjwa huo umeenea ndani ya vazi, ndani ya mtande, ndani ya mshindio, au ndani ya ngozi (haidhuru ngozi hiyo inatumiwa kwa kusudi gani), huo ni ukoma hatari, vazi hilo si safi.+ 52 Anapaswa kuliteketeza vazi hilo au mtande au mshindio wa sufu au wa kitani au kitu chochote cha ngozi kilichoathiriwa na ugonjwa huo, kwa sababu huo ni ukoma hatari. Ugonjwa huo unapaswa kuteketezwa.

53 “Lakini kuhani akichunguza na kuona kwamba ugonjwa haujaenea ndani ya vazi au ndani ya mtande au ndani ya mshindio au ndani ya kitu chochote cha ngozi, 54 ataamuru kitu kilichoathiriwa kioshwe, naye atakitenga kwa siku saba zaidi. 55 Baada ya kitu hicho kuoshwa kabisa, kuhani atakikagua. Ikiwa doa hilo halijabadilika, hata ikiwa ugonjwa haujaenea, kitu hicho si safi. Mnapaswa kukiteketeza kwa sababu kimeliwa na ukoma, iwe kimeliwa chini au ndani.

56 “Baada ya kitu hicho kuoshwa kabisa, kuhani atakikagua na akiona kwamba doa hilo limefifia, atararua sehemu iliyoathiriwa ya vazi au ngozi au mtande au mshindio. 57 Hata hivyo, doa hilo likitokea sehemu nyingine ya vazi au ndani ya mtande au ndani ya mshindio au ndani ya kitu chochote cha ngozi, ugonjwa huo unaenea, nanyi mnapaswa kuteketeza kitu chochote kilichoathiriwa.+ 58 Lakini ikiwa vazi au mtande au mshindio au kitu chochote cha ngozi hakina doa baada ya kuoshwa, kitu hicho kinapaswa kuoshwa mara ya pili, nacho kitakuwa safi.

59 “Hiyo ndiyo sheria kuhusu ugonjwa wa ukoma ulioathiri vazi la sufu au la kitani, au mtande au mshindio, au kitu chochote cha ngozi; itatumiwa kutangaza vitu hivyo kuwa safi au si safi.”

14 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Hii ndiyo sheria inayomhusu mtu mwenye ukoma ambayo inapaswa kufuatwa siku ambayo utakaso wake unathibitishwa, anapopelekwa kwa kuhani.+ 3 Kuhani atatoka nje ya kambi na kumchunguza. Ikiwa mtu mwenye ukoma amepona, 4 kuhani atamwamuru alete ndege safi wawili walio hai, tawi la mwerezi, kitambaa cha rangi nyekundu, na tawi la hisopo ili atakaswe.+ 5 Kuhani ataamuru ndege mmoja achinjwe kwenye chombo cha udongo chenye maji ya kijito. 6 Lakini anapaswa kumchukua ndege aliye hai na kumtumbukiza pamoja na tawi la mwerezi, kitambaa cha rangi nyekundu, na tawi la hisopo ndani ya damu ya ndege aliyechinjiwa kwenye maji ya kijito. 7 Kisha kuhani atachukua damu hiyo na kumnyunyizia mara saba mtu anayejitakasa ukoma wake na kumtangaza kuwa safi, halafu atamwachilia ndege aliye hai aende zake mashambani.+

8 “Ni lazima mtu anayejitakasa afue mavazi yake, anyoe nywele zake zote, na kuoga kwa maji, kisha atakuwa safi. Baada ya hayo, anaweza kurudi kambini, lakini atakaa nje ya hema lake kwa siku saba. 9 Siku ya saba anapaswa kunyoa nywele zote kichwani, ndevu zote, na kope zake. Baada ya kunyoa nywele zote, atafua mavazi yake na kuoga kwa maji, kisha atakuwa safi.

10 “Siku ya nane, ataleta wanakondoo dume wawili wasio na kasoro, mwanakondoo jike wa mwaka mmoja asiye na kasoro,+ na sehemu tatu za kumi za kipimo cha efa* ya unga laini uliochanganywa na mafuta kuwa toleo la nafaka,+ na logi moja* ya mafuta;+ 11 na kuhani anayemtangaza kuwa safi atamleta mtu huyo anayejitakasa na matoleo hayo mbele za Yehova kwenye mlango wa hema la mkutano. 12 Kuhani huyo atamchukua yule mwanakondoo dume na kumtoa kuwa dhabihu ya hatia+ pamoja na ile logi moja ya mafuta, naye atavitikisa kwenda mbele na nyuma vikiwa toleo la kutikiswa mbele za Yehova.+ 13 Kisha atamchinjia mwanakondoo huyo mahali ambapo dhabihu za dhambi na dhabihu za kuteketezwa huchinjwa,+ mahali patakatifu, kwa sababu, sawa na dhabihu ya dhambi, dhabihu ya hatia ni ya kuhani.+ Ni dhabihu takatifu kabisa.+

14 “Kisha kuhani atachukua kiasi kidogo cha damu ya dhabihu ya hatia na kupaka ncha ya sikio la kulia la mtu anayejitakasa na kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kidole gumba cha mguu wake wa kulia. 15 Halafu kuhani atachukua kiasi kidogo cha ile logi ya mafuta+ na kumimina kwenye kiganja chake mwenyewe cha mkono wa kushoto. 16 Kisha kuhani atachovya kidole chake cha kulia katika mafuta yaliyo kwenye kiganja chake cha kushoto, atanyunyiza mara saba kwa kidole chake kiasi kidogo cha mafuta hayo mbele za Yehova. 17 Kisha kuhani atatia kiasi kidogo cha mafuta yaliyobaki kwenye kiganja chake na kupaka ncha ya sikio la kulia la mtu anayejitakasa na kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kidole gumba cha mguu wake wa kulia juu ya damu ya dhabihu ya hatia. 18 Kuhani atatia mafuta yaliyobaki kwenye kiganja chake na kumpaka kichwani mtu anayejitakasa, naye kuhani atamtolea mtu huyo dhabihu ya kufunika dhambi yake mbele za Yehova.+

19 “Kuhani atatoa dhabihu ya dhambi+ na kumtolea dhabihu ya kufunika dhambi mtu anayejitakasa uchafu wake, kisha atamchinja mnyama wa dhabihu ya kuteketezwa. 20 Kuhani atatoa dhabihu ya kuteketezwa na toleo la nafaka+ kwenye madhabahu, naye atamtolea mtu huyo dhabihu ya kufunika dhambi yake,+ naye atakuwa safi.+

21 “Hata hivyo, ikiwa mtu huyo ni maskini na hawezi kupata vitu hivyo, basi ataleta mwanakondoo dume mmoja atolewe kuwa dhabihu ya hatia na toleo la kutikiswa, ili atoe dhabihu ya kufunika dhambi yake, pia ataleta sehemu ya kumi ya kipimo cha efa moja* ya unga laini uliochanganywa na mafuta ili uwe toleo la nafaka, logi ya mafuta, 22 na njiwa tetere wawili au hua wawili wachanga, kulingana na uwezo wake. Ndege mmoja atatolewa kuwa dhabihu ya dhambi na wa pili dhabihu ya kuteketezwa.+ 23 Siku ya nane+ atawaleta kwa kuhani kwenye mlango wa hema la mkutano mbele za Yehova ili kuthibitisha utakaso wake.+

24 “Kuhani atamchukua mwanakondoo dume wa dhabihu ya hatia+ na logi ya mafuta na kuvitikisa kwenda mbele na nyuma vikiwa toleo la kutikiswa mbele za Yehova.+ 25 Kisha atamchinja kondoo dume mchanga wa dhabihu ya hatia na kuchukua kiasi kidogo cha damu ya dhabihu ya hatia na kupaka ncha ya sikio la kulia la mtu anayejitakasa na kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kidole gumba cha mguu wake wa kulia.+ 26 Kuhani atamimina kiasi kidogo cha mafuta hayo kwenye kiganja chake mwenyewe cha mkono wa kushoto,+ 27 kisha atanyunyiza kwa kidole chake cha kulia kiasi kidogo cha mafuta yaliyo kwenye kiganja chake cha kushoto mara saba mbele za Yehova. 28 Naye atatia kiasi kidogo cha mafuta yaliyo kwenye kiganja chake na kupaka ncha ya sikio la kulia la mtu anayejitakasa na kidole gumba cha mkono wake wa kulia na kidole gumba cha mguu wake wa kulia sehemu zilezile alizompaka damu ya dhabihu ya hatia. 29 Kisha kuhani atatia mafuta yaliyobaki kwenye kiganja chake na kumpaka kichwani mtu anayejitakasa ili amtolee mtu huyo dhabihu ya kufunika dhambi yake mbele za Yehova.

30 “Atatoa njiwa tetere mmoja kati ya wale wawili au hua mmoja mchanga kati ya wale wawili, kulingana na uwezo wake,+ 31 atatoa ndege anaoweza kupata, mmoja kwa ajili ya dhabihu ya dhambi na mwingine kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa,+ ataleta pia toleo la nafaka; na kuhani atamtolea mtu huyo anayejitakasa dhabihu ya kufunika dhambi yake mbele za Yehova.+

32 “Hiyo ndiyo sheria inayomhusu mtu aliyekuwa na ugonjwa wa ukoma lakini hana uwezo wakati wa kuthibitisha utakaso wake.”

33 Kisha Yehova akamwambia Musa na Haruni: 34 “Mtakapoingia katika nchi ya Kanaani,+ ambayo ninawapa ili mwimiliki,+ nami niipige kwa ukoma nyumba fulani katika nchi yenu,+ 35 mwenye nyumba hiyo anapaswa kwenda kwa kuhani na kumwambia, ‘Nimeona madoa fulani ndani ya nyumba yangu.’ 36 Kuhani ataagiza vitu vyote vilivyo ndani ya nyumba hiyo vitolewe nje kabla hajaja kuikagua, ili asitangaze kwamba kila kitu kilicho katika nyumba hiyo si safi; baada ya hilo ataingia ndani na kuikagua. 37 Atachunguza sehemu zilizoathiriwa, na ikiwa kuta za nyumba hiyo zina sehemu zilizobonyea zenye mchanganyiko wa rangi ya manjano na kijani au rangi nyekundu, na sehemu hizo zinaonekana zimebonyea sana ukutani, 38 basi kuhani atatoka nje ya mlango wa nyumba hiyo na kuifunga kwa siku saba.+

39 “Kisha kuhani atarudi siku ya saba na kuikagua. Ikiwa madoa yameenea katika kuta za nyumba hiyo, 40 ndipo kuhani ataagiza mawe yaliyoathiriwa yabomolewe na kutupwa nje ya jiji, mahali pasipo safi. 41 Kisha ataagiza nyumba hiyo ikwanguliwe kabisa sehemu ya ndani, na lipu na saruji iliyoondolewa itatupwa nje ya jiji, mahali pasipo safi. 42 Kisha wataleta mawe mengine na kuyaweka mahali ambapo mawe ya kwanza yalikuwepo; anapaswa kutumia saruji nyingine kuipiga lipu nyumba hiyo.

43 “Hata hivyo, madoa yakitokea tena na kuenea ndani ya nyumba hiyo baada ya mawe kubomolewa na nyumba kukwanguliwa na kupigwa lipu tena, 44 kuhani ataingia ndani na kuikagua. Ikiwa madoa hayo yameenea, nyumba hiyo ina ukoma hatari.+ Si safi. 45 Ataagiza nyumba hiyo ibomolewe, yaani, mawe yake, mbao zake, na lipu yote katika nyumba hiyo, kisha vitu hivyo vitatupwa nje ya jiji, mahali pasipo safi.+ 46 Lakini mtu yeyote atakayeingia ndani ya nyumba hiyo siku yoyote itakapokuwa imetengwa,+ hatakuwa safi mpaka jioni;+ 47 na yeyote anayelala katika nyumba hiyo anapaswa kufua mavazi yake, na yeyote anayekula chakula katika nyumba hiyo anapaswa kufua mavazi yake.

48 “Hata hivyo, kuhani akija na kuona kwamba madoa hayajaenea baada ya nyumba hiyo kupigwa lipu tena, ataitangaza nyumba hiyo kuwa safi, kwa sababu ukoma umekwisha. 49 Ili kuitakasa nyumba hiyo isiyo safi,* atachukua ndege wawili, tawi la mwerezi, kitambaa cha rangi nyekundu, na tawi la hisopo.+ 50 Atamchinjia ndege mmoja kwenye chombo cha udongo chenye maji ya kijito. 51 Kisha atamchukua ndege aliye hai na kumtumbukiza pamoja na tawi la mwerezi, kitambaa cha rangi nyekundu, na tawi la hisopo ndani ya damu ya ndege aliyechinjiwa kwenye maji ya kijito, naye atainyunyiza kuelekea nyumba hiyo mara saba.+ 52 Naye ataitakasa nyumba hiyo isiyo safi* kwa kutumia damu ya ndege huyo, maji ya kijito, yule ndege aliye hai, tawi la mwerezi, tawi la hisopo, na kitambaa cha rangi nyekundu. 53 Kisha atamwachilia ndege aliye hai aende zake mashambani nje ya jiji, naye ataitolea nyumba hiyo dhabihu ya kufunika dhambi, nayo itakuwa safi.

54 “Hiyo ndiyo sheria kuhusu aina mbalimbali za ukoma: ukoma wa kichwa au kidevu,+ 55 ukoma wa mavazi+ au nyumba,+ 56 uvimbe, vigaga, na madoa,+ 57 ili kuthibitisha ikiwa kitu ni safi au si safi.+ Hiyo ndiyo sheria kuhusu ukoma.”+

15 Yehova akaendelea kuwaambia Musa na Haruni: 2 “Waambieni Waisraeli, ‘Mwanamume akitokwa na umajimaji kwenye kiungo chake cha uzazi,* umajimaji huo unamfanya asiwe safi.+ 3 Yeye si safi kwa sababu ya umajimaji huo, iwe umajimaji huo unaendelea kutoka katika kiungo chake cha uzazi au umezuiwa kutoka, bado yeye si safi.

4 “‘Kitanda chochote anacholalia mtu anayetokwa na umajimaji hakitakuwa safi, na kitu chochote anachokalia hakitakuwa safi. 5 Mtu anayegusa kitanda cha mtu huyo ni lazima afue mavazi yake na kuoga kwenye maji, naye hatakuwa safi mpaka jioni.+ 6 Mtu yeyote anayeketi kwenye kitu kilichokaliwa na mtu anayetokwa na umajimaji anapaswa kufua mavazi yake na kuoga kwenye maji, naye hatakuwa safi mpaka jioni. 7 Mtu yeyote anayemgusa mtu anayetokwa na umajimaji anapaswa kufua mavazi yake na kuoga kwenye maji, naye hatakuwa safi mpaka jioni. 8 Mtu anayetokwa na umajimaji akimtemea mate mtu aliye safi, ni lazima mtu aliyetemewa mate ayafue mavazi yake na kuoga kwenye maji, naye hatakuwa safi mpaka jioni. 9 Matandiko yoyote yaliyo mgongoni mwa mnyama yatakayokaliwa na mtu anayetokwa na umajimaji hayatakuwa safi. 10 Mtu yeyote anayegusa kitu chochote kilichokaliwa na mtu huyo hatakuwa safi mpaka jioni, na yeyote anayebeba vitu hivyo atafua mavazi yake na kuoga kwenye maji, naye hatakuwa safi mpaka jioni. 11 Mtu anayetokwa na umajimaji+ akimgusa mtu mwingine bila kunawa mikono, ni lazima mtu aliyeguswa afue mavazi yake na kuoga kwenye maji, naye hatakuwa safi mpaka jioni. 12 Chombo cha udongo kinachoguswa na mtu anayetokwa na umajimaji kinapaswa kuvunjwa, na chombo chochote cha mbao kinapaswa kusafishwa kwa maji.+

13 “‘Mtu aliyekuwa akitokwa na umajimaji akipona na kuwa safi, atangoja kwa siku saba ili atakaswe, na ni lazima afue mavazi yake na kuoga kwenye maji ya kijito, naye atakuwa safi.+ 14 Siku ya nane, anapaswa kuchukua njiwa tetere wawili au hua wawili wachanga+ na kwenda mbele za Yehova, kwenye mlango wa hema la mkutano na kumpa kuhani ndege hao. 15 Kisha kuhani atamtoa ndege mmoja kwa ajili ya dhabihu ya dhambi na ndege wa pili kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa, naye kuhani atamtolea mtu huyo dhabihu ya kufunika dhambi yake mbele za Yehova ili awe safi kutokana na umajimaji wake.

16 “‘Mwanamume akitokwa na shahawa, anapaswa kuoga mwili mzima kwenye maji naye hatakuwa safi mpaka jioni.+ 17 Ni lazima afue kwa maji vazi lolote na ngozi yoyote iliyomwagikiwa na shahawa, na vitu hivyo havitakuwa safi mpaka jioni.

18 “‘Mwanamume akilala na mwanamke kisha atokwe na shahawa, wote wawili wanapaswa kuoga kwenye maji na hawatakuwa safi mpaka jioni.+

19 “‘Ikiwa mwanamke anatokwa na damu ya hedhi, hatakuwa safi kwa siku saba.+ Mtu yeyote anayemgusa hatakuwa safi mpaka jioni.+ 20 Kitu chochote anacholalia muda wote ambao yeye si safi kwa sababu ya hedhi hakitakuwa safi, na kila kitu anachokalia hakitakuwa safi.+ 21 Mtu yeyote anayegusa kitanda chake anapaswa kufua mavazi yake na kuoga kwenye maji, naye hatakuwa safi mpaka jioni. 22 Mtu yeyote anayegusa kitu chochote alichokalia mwanamke huyo anapaswa kufua mavazi yake na kuoga kwenye maji, naye hatakuwa safi mpaka jioni. 23 Ikiwa mwanamke huyo aliketi kwenye kitanda au kitu kingine, mwanamume anayekigusa hatakuwa safi mpaka jioni.+ 24 Mwanamume akilala na mwanamke huyo kisha damu ya hedhi imguse,+ mwanamume huyo hatakuwa safi kwa siku saba, na kitanda chochote anacholalia hakitakuwa safi.

25 “‘Mwanamke akitokwa na damu kwa siku nyingi+ wakati ambao si wa hedhi,+ au akitokwa na damu kwa muda unaozidi kipindi chake cha hedhi, hatakuwa safi sikuzote anazotokwa na damu, kama tu inavyokuwa wakati wa hedhi. 26 Kitanda chochote anacholalia na kitu chochote anachokalia anapotokwa na damu hakitakuwa safi,+ kitakuwa kama kinavyokuwa wakati wa hedhi. 27 Mtu yeyote anayegusa vitu hivyo hatakuwa safi, ni lazima afue mavazi yake na kuoga kwenye maji, naye hatakuwa safi mpaka jioni.+

28 “‘Hata hivyo, damu yake ikiacha kutoka, atahesabu siku saba, na baada ya siku hizo atakuwa safi.+ 29 Siku ya nane, atachukua njiwa tetere wawili au hua wawili wachanga+ na kumpelekea kuhani kwenye mlango wa hema la mkutano.+ 30 Kuhani atamtoa ndege mmoja kwa ajili ya dhabihu ya dhambi na ndege wa pili kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa, kisha atamtolea mwanamke huyo dhabihu ya kufunika dhambi yake mbele za Yehova ili awe safi kutokana na damu yake.+

31 “‘Kwa hiyo ni lazima muwalinde Waisraeli waepuke uchafu wao, ili wasife katika uchafu wao kwa kulitia unajisi hema langu la ibada ambalo liko kati yao.+

32 “‘Hiyo ndiyo sheria kuhusu mtu anayetokwa na umajimaji, mwanamume asiye safi kwa sababu ya kutokwa na shahawa,+ 33 mwanamke asiye safi kwa sababu ya hedhi,+ mwanamume au mwanamke yeyote anayetokwa na umajimaji mwilini,+ na mwanamume anayelala na mwanamke asiye safi.’”

16 Yehova akazungumza na Musa baada ya wana wawili wa Haruni kufa kwa sababu ya kumkaribia Yehova.+ 2 Yehova akamwambia Musa: “Mwambie Haruni ndugu yako asiingie mahali patakatifu+ nyuma ya pazia+ mbele ya kifuniko cha sanduku la agano wakati wowote tu, asije akafa,+ kwa sababu nitatokea katika wingu juu ya kifuniko hicho.+

3 “Hivi ndivyo vitu ambavyo Haruni anapaswa kuleta anapoingia mahali patakatifu: ng’ombe dume mchanga kwa ajili ya dhabihu ya dhambi+ na kondoo dume kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa.+ 4 Anapaswa kuvaa kanzu takatifu ya kitani,+ na suruali fupi*+ ya kitani inapaswa kufunika mwili wake,* na anapaswa kujifunga ukumbuu wa kitani+ na kuvaa kilemba cha kitani+ kichwani. Ni mavazi matakatifu.+ Ataoga kwenye maji+ na kuyavaa.

5 “Anapaswa kuchukua kutoka kwa Waisraeli+ wanambuzi dume wawili kwa ajili ya dhabihu ya dhambi na kondoo dume mmoja kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa.

6 “Kisha Haruni atamtoa yule ng’ombe dume wa dhabihu ya dhambi kwa ajili yake mwenyewe, naye atatoa dhabihu ya kufunika dhambi zake mwenyewe+ na za nyumba yake.

7 “Halafu atachukua wale mbuzi wawili na kuwapeleka mbele za Yehova kwenye mlango wa hema la mkutano. 8 Haruni atapiga kura kwa ajili ya mbuzi hao wawili, kura moja ya Yehova na nyingine ya Azazeli.* 9 Haruni atamchukua yule mbuzi aliyechaguliwa kwa kura+ kuwa wa Yehova na kutoa dhabihu ya dhambi. 10 Lakini yule mbuzi aliyechaguliwa kwa kura kuwa wa Azazeli anapaswa kupelekwa akiwa hai mbele za Yehova ili dhabihu ya kufunika dhambi itolewe juu yake, kusudi aachiliwe aende zake nyikani+ akiwa wa Azazeli.

11 “Haruni atamtoa yule ng’ombe dume wa dhabihu ya dhambi, ambaye anatolewa kwa ajili yake mwenyewe, na kutoa dhabihu ya kufunika dhambi zake mwenyewe na za nyumba yake; kisha atamchinja ng’ombe dume huyo wa dhabihu ya dhambi, anayetolewa kwa ajili yake mwenyewe.+

12 “Halafu atachukua chetezo+ kilichojaa makaa ya moto kutoka katika madhabahu+ mbele za Yehova na mikono miwili iliyojaa uvumba bora uliotiwa manukato,+ naye ataleta vitu hivyo nyuma ya pazia.+ 13 Pia atatia uvumba huo juu ya moto mbele za Yehova,+ na moshi wa uvumba huo utafunika kifuniko cha sanduku la agano,+ kilicho juu ya ule Ushahidi,+ asije akafa.

14 “Atachukua kiasi fulani cha damu ya ng’ombe dume+ na kuinyunyiza kwa kidole chake mbele ya kifuniko upande wa mashariki, atanyunyiza kiasi fulani cha damu hiyo mara saba mbele ya kifuniko hicho.+

15 “Kisha atamchinja yule mbuzi wa dhabihu ya dhambi kwa ajili ya watu+ na kuleta damu yake nyuma ya pazia,+ atafanya kama alivyofanya na damu+ ya yule ng’ombe dume; atainyunyiza kuelekea hicho kifuniko na mbele ya hicho kifuniko.

16 “Ni lazima atoe dhabihu ya kufunika dhambi kwa ajili ya mahali patakatifu kwa sababu ya uchafu, makosa, na dhambi za Waisraeli,+ na hivyo ndivyo anavyopaswa kufanya kwa ajili ya hema la mkutano ambalo liko miongoni mwao katikati ya uchafu wao.

17 “Hakuna mtu mwingine yeyote anayepaswa kuwa ndani ya hema la mkutano kuanzia wakati Haruni anapoingia mahali patakatifu kutoa dhabihu ya kufunika dhambi, mpaka anapotoka nje. Atatoa dhabihu ya kufunika dhambi zake mwenyewe na za nyumba yake+ na za kusanyiko lote la Waisraeli.+

18 “Kisha atatoka nje na kwenda kwenye madhabahu+ iliyo mbele za Yehova, naye atatoa dhabihu ya kufunika dhambi kwa ajili ya madhabahu hiyo, kisha atachukua kiasi fulani cha damu ya yule ng’ombe dume na kiasi fulani cha damu ya yule mbuzi na kupaka pembe za madhabahu pande zote. 19 Pia atainyunyizia madhabahu kiasi fulani cha damu hiyo mara saba kwa kidole chake na kuisafisha na kuitakasa kwa sababu ya uchafu wa Waisraeli.

20 “Baada ya kutoa dhabihu ya kufunika dhambi+ kwa ajili ya mahali patakatifu, hema la mkutano, na madhabahu,+ atamtoa pia yule mbuzi aliye hai.+ 21 Haruni ataweka mikono yake miwili juu ya kichwa cha mbuzi huyo aliye hai na kuungama juu yake makosa yote ya Waisraeli na maovu yao yote na dhambi zao zote, ataziweka juu ya kichwa cha mbuzi+ huyo na kumwagiza mtu aliyechaguliwa* ampeleke mbuzi huyo nyikani. 22 Mbuzi huyo atazibeba dhambi zao zote+ na kuzipeleka jangwani,+ mtu huyo atampeleka mbuzi huyo na kumwacha aende zake nyikani.+

23 “Kisha Haruni ataingia katika hema la mkutano na kuyavua yale mavazi ya kitani aliyovaa alipoingia mahali patakatifu, naye atayaweka chini humo. 24 Ni lazima aoge mwili wake kwa maji+ mahali patakatifu na kuvaa mavazi yake;+ kisha atatoka nje na kutoa dhabihu yake ya kuteketezwa+ na dhabihu ya watu ya kuteketezwa;+ atatoa dhabihu ya kufunika dhambi zake mwenyewe na za watu wote.+ 25 Atayateketeza mafuta ya dhabihu ya dhambi ili yafuke moshi kwenye madhabahu.

26 “Yule mtu aliyempeleka mbuzi wa Azazeli+ anapaswa kufua mavazi yake na kuoga kwenye maji, kisha anaweza kurudi kambini.

27 “Yule ng’ombe dume wa dhabihu ya dhambi na yule mbuzi wa dhabihu ya dhambi, ambao damu yao ililetwa mahali patakatifu ili itumiwe kufunika dhambi, watapelekwa nje ya kambi, na ngozi zao na nyama yao na mavi yao vitateketezwa motoni.+ 28 Mtu atakayeteketeza vitu hivyo anapaswa kufua mavazi yake na kuoga kwenye maji, kisha anaweza kurudi kambini.

29 “Ifuatayo itakuwa sheria ya kudumu kwa ajili yenu: Katika mwezi wa saba, siku ya kumi ya mwezi huo, mnapaswa kujitesa,* hampaswi kufanya kazi yoyote,+ awe ni mwenyeji au mgeni anayeishi miongoni mwenu. 30 Siku hiyo dhabihu ya kufunika dhambi+ itatolewa kwa ajili yenu ili mtangazwe kuwa safi. Mtasafishwa dhambi zenu zote mbele za Yehova.+ 31 Ni sabato ya pumziko kamili kwenu, mnapaswa kujitesa.*+ Ni sheria ya kudumu.

32 “Kuhani atakayetiwa mafuta+ na kuwekwa rasmi*+ ili atumike akiwa kuhani baada ya baba yake,+ atatoa dhabihu ya kufunika dhambi na kuvaa yale mavazi matakatifu+ ya kitani.+ 33 Atatoa dhabihu ya kufunika dhambi kwa ajili ya mahali patakatifu,+ hema la mkutano,+ na madhabahu;+ naye atatoa dhabihu ya kufunika dhambi za makuhani na za watu wote.+ 34 Hiyo itakuwa sheria ya kudumu kwa ajili yenu+ ili dhabihu ya kufunika dhambi itolewe kwa ajili ya Waisraeli ili kufunika dhambi zao zote mara moja kila mwaka.”+

Basi Haruni akafanya kama Yehova alivyomwamuru Musa.

17 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Mwambie Haruni na wanawe na Waisraeli wote, ‘Yehova ameamuru hivi:

3 “‘“Mwisraeli yeyote akimchinja ng’ombe dume au mwanakondoo dume au mbuzi ndani au nje ya kambi, 4 na kukosa kumleta kwenye mlango wa hema la mkutano ili kumtolea Yehova dhabihu mbele ya hema la Yehova la ibada, mtu huyo atakuwa na hatia ya damu. Ameua,* naye ni lazima auawe. 5 Itakuwa hivyo ili Waisraeli wamletee Yehova dhabihu wanazotolea mashambani, wamletee kuhani dhabihu hizo kwenye mlango wa hema la mkutano. Wanapaswa kumtolea Yehova dhabihu hizo zikiwa dhabihu za ushirika.+ 6 Naye kuhani atainyunyizia madhabahu ya Yehova damu ya dhabihu hizo kwenye mlango wa hema la mkutano na kuteketeza mafuta yake ili yafuke moshi yakiwa harufu inayompendeza* Yehova.+ 7 Kwa hiyo hawapaswi tena kutoa dhabihu zao kwa roho waovu wenye umbo la mbuzi,*+ wanaofanya nao ukahaba.+ Hiyo itakuwa sheria ya kudumu kwa ajili yenu katika vizazi vyenu vyote.”’

8 “Waambie hivi: ‘Mwisraeli yeyote au mgeni yeyote anayeishi miongoni mwenu atakayetoa dhabihu ya kuteketezwa au dhabihu yoyote 9 na kukosa kuileta kwenye mlango wa hema la mkutano ili kumtolea Yehova ni lazima auawe.+

10 “‘Mwisraeli yeyote au mgeni yeyote anayeishi miongoni mwenu akila damu yoyote ile,+ kwa hakika nitamkataa* mtu anayekula damu, nami nitamwangamiza atoke miongoni mwa watu wake. 11 Kwa maana uhai wa kiumbe umo* katika damu,+ nami nimeitoa kwenye madhabahu+ ili mwitumie kufunika dhambi zenu, kwa maana damu ndiyo inayofunika dhambi+ kupitia uhai ulio ndani yake. 12 Ndiyo sababu nimewaambia Waisraeli hivi: “Hakuna yeyote kati yenu anayepaswa kula damu, na hakuna mgeni yeyote anayeishi miongoni mwenu+ anayepaswa kula damu.”+

13 “‘Mwisraeli yeyote au mgeni yeyote anayeishi miongoni mwenu akiwinda na kumkamata mnyama wa mwituni au ndege anayeweza kuliwa, ni lazima amwage damu yake+ chini na kuifunika kwa udongo. 14 Kwa maana uhai wa* kila kiumbe ni damu yake, kwa sababu uhai umo* ndani ya damu. Kwa hiyo, niliwaambia Waisraeli: “Hampaswi kula damu ya kiumbe yeyote kwa sababu uhai wa kila kiumbe umo katika damu yake. Mtu yeyote anayekula damu atauawa.”+ 15 Mtu yeyote, awe ni mwenyeji au mgeni, akila mnyama aliyepatikana amekufa au aliyeraruliwa na mnyama wa mwituni,+ basi ni lazima afue mavazi yake na kuoga kwenye maji,+ naye hatakuwa safi mpaka jioni. 16 Lakini asipofua mavazi yake na kuoga, atawajibika kwa sababu ya kosa lake.’”+

18 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Waambie Waisraeli hivi: ‘Mimi ni Yehova Mungu wenu.+ 3 Msifanye kama wanavyofanya katika nchi ya Misri ambako mliishi, wala msifanye kama wanavyofanya katika nchi ya Kanaani ambako nawapeleka.+ Msifuate sheria zao. 4 Mnapaswa kutekeleza sheria zangu,* nanyi mnapaswa kutii amri zangu na kuzifuata.+ Mimi ni Yehova Mungu wenu. 5 Ni lazima mshike amri zangu na sheria zangu;* yeyote anayefanya hivyo ataishi kupitia hizo.+ Mimi ni Yehova.

6 “‘Hakuna mtu yeyote kati yenu anayepaswa kumkaribia mtu wake wa karibu wa ukoo ili kufanya naye ngono.*+ Mimi ni Yehova. 7 Usifanye ngono na baba yako wala mama yako. Yeye ni mama yako, usifanye naye ngono.

8 “‘Usifanye ngono na mke wa baba yako.+ Utamwaibisha baba yako.*

9 “‘Usifanye ngono na dada yako, awe ni binti ya baba yako au binti ya mama yako, awe amezaliwa katika nyumba ileile au amezaliwa nje.+

10 “‘Usifanye ngono na binti ya mwana wako au binti ya binti yako, kwa sababu ni uchi wako mwenyewe.

11 “‘Usifanye ngono na binti ya mke wa baba yako, mtoto wa baba yako, kwa sababu ni dada yako.

12 “‘Usifanye ngono na dada ya baba yako. Ana uhusiano wa damu na baba yako.+

13 “‘Usifanye ngono na dada ya mama yako, kwa sababu ana uhusiano wa damu na mama yako.

14 “‘Usimwaibishe* ndugu ya baba yako kwa kufanya ngono na mke wake. Mke huyo ni shangazi yako.+

15 “‘Usifanye ngono na binti mkwe wako.+ Yeye ni mke wa mwana wako, usifanye naye ngono.

16 “‘Usifanye ngono na mke wa ndugu yako,+ kwa sababu utamwaibisha ndugu yako.*

17 “‘Usifanye ngono na mwanamke na binti yake.+ Usimchukue binti ya mwana wa mwanamke huyo na binti ya binti yake ili kufanya nao ngono. Wao ni watu wake wa karibu wa ukoo; hilo ni tendo chafu linalochukiza.*

18 “‘Usimchukue dada ya mke wako ili awe mke mwenza+ na kufanya naye ngono wakati mke wako angali hai.

19 “‘Usimkaribie mwanamke wakati wa hedhi anapokuwa si safi ili kufanya naye ngono.+

20 “‘Usifanye ngono na mke wa jirani yako* na hivyo kujichafua.+

21 “‘Usikubali mtoto wako yeyote atolewe dhabihu kwa Moleki.+ Usilichafue jina la Mungu wako kwa njia hiyo.+ Mimi ni Yehova.

22 “‘Usilale na mwanamume kama vile unavyolala na mwanamke.+ Ni tendo linalochukiza.

23 “‘Mwanamume hapaswi kujichafua kwa kufanya ngono na mnyama; wala mwanamke hapaswi kwenda kufanya ngono na mnyama.+ Kufanya hivyo kunakiuka sheria ya asili.

24 “‘Msijichafue kwa kufanya jambo lolote kati ya mambo hayo, kwa maana mataifa ninayoyafukuza kutoka mbele yenu yamejichafua kwa mambo hayo yote.+ 25 Kwa hiyo nchi si safi, nami nitaiadhibu kwa sababu ya dhambi yake, nayo nchi itawatapika wakaaji wake.+ 26 Lakini ni lazima ninyi mzishike amri zangu na sheria zangu,*+ msifanye jambo lolote kati ya mambo hayo yenye kuchukiza, awe ni mwenyeji au mgeni anayeishi miongoni mwenu.+ 27 Kwa maana mambo hayo yote yenye kuchukiza yalifanywa na watu walioishi katika nchi hiyo kabla yenu,+ na sasa nchi si safi. 28 Msifanye mambo hayo ili nchi isiwatapike kwa sababu ya kuichafua kama itakavyoyatapika mataifa yaliyowatangulia. 29 Mtu yeyote akifanya jambo lolote kati ya mambo hayo yenye kuchukiza, wote wanaofanya mambo hayo ni lazima wauawe watoke miongoni mwa watu wao. 30 Ni lazima mtimize wajibu wenu kwangu kwa kutofuata desturi yoyote kati ya desturi zenye kuchukiza zilizofuatwa kabla yenu,+ ili msijichafue kwa desturi hizo. Mimi ni Yehova Mungu wenu.’”

19 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Waambie hivi Waisraeli wote: ‘Mnapaswa kuwa watakatifu, kwa sababu mimi, Yehova Mungu wenu, ni mtakatifu.+

3 “‘Kila mmoja wenu anapaswa kumheshimu* mama yake na baba yake,+ nanyi mnapaswa kushika sabato zangu.+ Mimi ni Yehova Mungu wenu. 4 Msiigeukie miungu ya ubatili+ wala msijitengenezee miungu ya chuma.+ Mimi ni Yehova Mungu wenu.

5 “‘Mnaponitolea mimi Yehova dhabihu ya ushirika,+ mnapaswa kuitoa kwa njia itakayofanya mpate kibali.+ 6 Inapaswa kuliwa siku inayotolewa na siku inayofuata, lakini siku ya tatu, dhabihu inayobaki inapaswa kuteketezwa.+ 7 Hata hivyo, ikiwa dhabihu yoyote inayobaki italiwa siku ya tatu, ni chukizo na haitakubaliwa. 8 Mtu anayeila ataadhibiwa kwa sababu ya kosa lake kwa maana amechafua kitu kitakatifu cha Yehova, naye lazima auawe.

9 “‘Mnapovuna mashamba yenu, msivune kabisa ukingo wa mashamba yenu, nanyi msiokote masalio ya mavuno yenu.+ 10 Pia, msikusanye masalio ya mashamba yenu ya mizabibu wala msiokote zabibu zilizoanguka chini. Waachieni maskini*+ na wageni. Mimi ni Yehova Mungu wenu.

11 “‘Msiibe,+ msidanganye,+ wala msitendeane kwa hila. 12 Msiape kwa uwongo kwa jina langu+ na hivyo kulichafua jina la Mungu wenu. Mimi ni Yehova. 13 Usimlaghai mwenzako+ wala kumnyang’anya vitu vyake.+ Usikae na mshahara wa kibarua usiku kucha mpaka asubuhi.+

14 “‘Usimtukane* kiziwi wala kuweka kizuizi mbele ya kipofu,+ nawe ni lazima umwogope Mungu wako.+ Mimi ni Yehova.

15 “‘Usitoe hukumu isiyo ya haki. Usiwabague maskini au kuwapendelea matajiri.+ Unapaswa kumhukumu mwenzako kwa haki.

16 “‘Usizungukezunguke kati ya watu wako ukieneza uchongezi.+ Usihatarishe uhai wa* mwenzako.+ Mimi ni Yehova.

17 “‘Usimchukie ndugu yako moyoni mwako.+ Lazima umkaripie mwenzako,+ usije ukashiriki dhambi yake.

18 “‘Usilipize kisasi+ wala usiwe na kinyongo dhidi ya wana wa watu wako, ni lazima umpende mwenzako kama unavyojipenda mwenyewe.+ Mimi ni Yehova.

19 “‘Mnapaswa kushika sheria zangu: Usiwaache wanyama wako wa kufugwa wazaane na wanyama wengine wa aina tofauti. Usipande mbegu za aina mbili+ katika shamba lako, na usivae vazi lililoshonwa kwa nyuzi za aina mbili.+

20 “‘Mwanamume akifanya ngono na kijakazi anayechumbiwa na mwanamume mwingine, na iwe kwamba kijakazi huyo hajakombolewa wala kuwekwa huru, wanapaswa kuadhibiwa. Hata hivyo, hawapaswi kuuawa, kwa sababu kijakazi huyo hakuwa amewekwa huru. 21 Mwanamume huyo anapaswa kumletea Yehova dhabihu yake ya hatia kwenye mlango wa hema la mkutano, kondoo dume wa dhabihu ya hatia.+ 22 Kuhani atamtoa kondoo dume huyo wa dhabihu ya hatia ili kufunika dhambi ya mwanamume huyo mbele za Yehova, naye atasamehewa dhambi aliyotenda.

23 “‘Mtakapofika katika nchi hiyo na kupanda mti wowote wa matunda, mnapaswa kuyaona matunda yake kuwa machafu na yaliyokatazwa.* Kwa miaka mitatu mmekatazwa kuyala.* Hayapaswi kuliwa. 24 Lakini katika mwaka wa nne, matunda yake yote yatakuwa matakatifu, mtamtolea Yehova kwa shangwe.+ 25 Kisha katika mwaka wa tano, mnaweza kula matunda yake ili kuongeza mazao yake kwenye mavuno yenu. Mimi ni Yehova Mungu wenu.

26 “‘Msile kitu chochote kilicho na damu.+

“‘Msitafute ishara za ubashiri au kufanya uchawi.+

27 “‘Msinyoe* masharafa yenu au kuharibu kingo za ndevu zenu.+

28 “‘Msijikatekate mwilini kwa ajili ya mtu aliyekufa,*+ nanyi msijichanje chale. Mimi ni Yehova.

29 “‘Usimwaibishe binti yako kwa kumfanya kuwa kahaba,+ ili nchi isifanye ukahaba na kujaa upotovu wa maadili.+

30 “‘Ni lazima mshike sabato zangu,+ nanyi mnapaswa kuheshimu* mahali pangu patakatifu. Mimi ni Yehova.

31 “‘Msiende kwa watu wanaowasiliana na roho,+ wala msitafute ushauri kutoka kwa wabashiri+ msije mkajichafua. Mimi ni Yehova Mungu wenu.

32 “‘Unapaswa kuinuka mbele ya kichwa chenye mvi,+ na ni lazima umheshimu mzee,+ nawe lazima umwogope Mungu wako.+ Mimi ni Yehova.

33 “‘Mgeni akiishi nanyi katika nchi yenu, msimtese.+ 34 Mgeni anayeishi pamoja nanyi mtamwona kama mwenyeji;+ nanyi lazima mumpende kama mnavyojipenda wenyewe, kwa maana mlikuwa wageni nchini Misri.+ Mimi ni Yehova Mungu wenu.

35 “‘Msitumie vipimo vya uwongo kupima urefu, uzito, au ujazo.+ 36 Mnapaswa kutumia mizani sahihi, vipimo sahihi, kipimo sahihi cha vitu vikavu,* na kipimo sahihi cha vitu vya majimaji.*+ Mimi ni Yehova Mungu wenu niliyewatoa katika nchi ya Misri. 37 Kwa hiyo ni lazima mshike masharti yangu yote na sheria zangu zote,* mnapaswa kuzifuata.+ Mimi ni Yehova.’”

20 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Waambie hivi Waisraeli: ‘Mwanamume yeyote Mwisraeli na mgeni yeyote anayeishi katika nchi ya Israeli atakayemtoa mtoto wake dhabihu kwa Moleki ni lazima auawe.+ Watu wote wanapaswa kumuua kwa kumpiga mawe. 3 Mimi mwenyewe nitamkataa* mtu huyo, nami nitamwangamiza, kwa sababu amemtoa mtoto wake dhabihu kwa Moleki, ametia unajisi mahali pangu patakatifu+ na kulichafua jina langu takatifu. 4 Watu wakimwona mtu huyo akimtoa mtoto wake dhabihu kwa Moleki na wakatae kimakusudi kumuua mtu huyo,+ 5 basi mimi mwenyewe nitamkataa* mtu huyo pamoja na familia yake.+ Nitamwangamiza pamoja na wote waliojiunga naye kufanya ukahaba na Moleki.

6 “‘Kwa hakika nitamkataa na kumwangamiza mtu yeyote anayetafuta ushauri kutoka kwa watu wanaowasiliana na roho+ na pia wabashiri+ ili kufanya ukahaba wa kiroho pamoja nao.+

7 “‘Ni lazima mjitakase na kuwa watakatifu,+ kwa sababu mimi ni Yehova Mungu wenu. 8 Nanyi lazima mshike sheria zangu na kuzifuata.+ Mimi ni Yehova, ninayewatakasa.+

9 “‘Mtu yeyote anayemtukana* baba yake au mama yake lazima auawe.+ Kwa kuwa amemtukana baba yake au mama yake atakuwa na hatia kwa sababu ya kifo chake mwenyewe.*

10 “‘Ifuatayo ni sheria kuhusu mwanamume anayefanya uzinzi na mke wa mwanamume mwingine: Mwanamume anayefanya uzinzi na mke wa mwenzake lazima auawe; mwanamume huyo na mwanamke aliyefanya naye uzinzi lazima wauawe.+ 11 Mwanamume anayefanya ngono na mke wa baba yake amemwaibisha baba yake.*+ Ni lazima wote wawili wauawe. Watakuwa na hatia kwa sababu ya vifo vyao wenyewe.* 12 Mwanamume akifanya ngono na binti mkwe wake, wote wawili wanapaswa kuuawa. Wamekiuka sheria ya asili. Watakuwa na hatia kwa sababu ya vifo vyao wenyewe.*+

13 “‘Mwanamume akilala na mwanamume mwenzake kama vile mwanamume anavyolala na mwanamke, wote wawili wamefanya jambo linalochukiza.+ Ni lazima wauawe. Watakuwa na hatia kwa sababu ya vifo vyao wenyewe.*

14 “‘Mwanamume akimwoa mwanamke na afanye ngono na mama ya mwanamke huyo, ni tendo chafu linalochukiza.*+ Anapaswa kuchomwa moto+ pamoja na wanawake hao, ili mwenendo huo mchafu unaochukiza usiendelee miongoni mwenu.

15 “‘Mwanamume akifanya ngono na mnyama lazima auawe, mnapaswa pia kumuua mnyama huyo.+ 16 Mwanamke akienda kufanya ngono na mnyama,+ ni lazima mumuue mwanamke huyo pamoja na mnyama huyo. Lazima wauawe. Watakuwa na hatia kwa sababu ya vifo vyao wenyewe.*

17 “‘Mwanamume akifanya ngono na dada yake, binti ya baba yake au binti ya mama yake na kuona uchi wake na binti huyo pia aone uchi wake, ni jambo la aibu.+ Ni lazima wauawe mbele ya watu wote. Amemwaibisha dada yake.* Anapaswa kuadhibiwa.

18 “‘Mwanamume akifanya ngono na mwanamke mwenye hedhi, mwanamume huyo na mwanamke huyo wamefunua mtiririko wa damu yake.+ Ni lazima wote wawili wauawe.

19 “‘Hupaswi kufanya ngono na dada ya mama yako au dada ya baba yako, kwa sababu kufanya hivyo ni kumwaibisha mtu wako wa ukoo uliye na uhusiano wa damu naye.+ Wanapaswa kuadhibiwa kwa sababu ya kosa lao. 20 Mwanamume anayefanya ngono na mke wa ndugu ya baba yake amemwaibisha* ndugu ya baba yake.+ Wanapaswa kuadhibiwa kwa sababu ya dhambi yao. Watakufa bila watoto. 21 Mwanamume akimchukua mke wa ndugu yake, ni jambo linalochukiza sana.+ Amemwaibisha ndugu yake.* Hawatazaa mtoto.

22 “‘Ni lazima mshike masharti yangu yote na sheria zangu zote+ na kuzifuata,+ ili nchi ninayowapa mwishi ndani yake isiwatapike.+ 23 Hampaswi kufuata sheria za mataifa ninayoyafukuza kutoka mbele yenu;+ kwa sababu yamefanya mambo hayo yote, nami ninayachukia kabisa mataifa hayo.+ 24 Ndiyo sababu niliwaambia: “Mtaimiliki nchi yao, nami nitawapa iwe miliki yenu, nchi inayotiririka maziwa na asali.+ Mimi ni Yehova Mungu wenu, nami nimewatenga na mataifa mengine.”+ 25 Ni lazima mtofautishe mnyama aliye safi na asiye safi na ndege aliye safi na asiye safi;+ msinifanye niwachukie kwa kula mnyama au ndege au kiumbe yeyote anayetambaa niliyewaambia kwamba si safi.+ 26 Ni lazima muwe watakatifu mbele zangu, kwa sababu mimi, Yehova, ni mtakatifu,+ nami ninawatenga na mataifa mengine ili muwe watu wangu.+

27 “‘Mwanamume au mwanamke yeyote ambaye anawasiliana na roho au ni mbashiri* lazima auawe.+ Watu wanapaswa kuwaua kwa kuwapiga mawe. Watakuwa na hatia kwa sababu ya vifo vyao wenyewe.’”*

21 Yehova akaendelea kumwambia Musa: “Waambie hivi wana wa Haruni, makuhani: ‘Mtu yeyote kati yenu asijichafue kwa kumgusa mtu aliyekufa* miongoni mwa watu wake.+ 2 Lakini anaweza kufanya hivyo kwa ajili ya mtu wa karibu wa ukoo aliye na uhusiano wa damu naye, mama yake, baba yake, mwana wake, binti yake, ndugu yake, 3 na anaweza kujichafua kwa kumgusa dada yake wa karibu ikiwa ni bikira na hajaolewa. 4 Hapaswi kujichafua na kujitia unajisi kwa kumgusa mke wa mwanamume anayetoka katika ukoo wake. 5 Hawapaswi kunyoa upara+ au kukata ncha za ndevu zao au kujikatakata mwilini.+ 6 Wanapaswa kuwa watakatifu mbele za Mungu wao,+ nao hawapaswi kulichafua jina la Mungu wao,+ kwa sababu wanatoa dhabihu za Yehova zinazochomwa kwa moto, mkate wa* Mungu wao, lazima wawe watakatifu.+ 7 Hawapaswi kumwoa kahaba,+ mwanamke aliyenajisiwa, au mwanamke aliyetalikiwa na mume wake,+ kwa sababu kuhani ni mtakatifu mbele za Mungu wake. 8 Ni lazima umtakase kuhani,+ kwa sababu ndiye anayetoa mkate wa Mungu wenu. Mnapaswa kumwona kuwa mtakatifu, kwa sababu mimi, Yehova, ninayewatakasa ninyi, ni mtakatifu.+

9 “‘Sasa binti ya kuhani akijichafua kwa kufanya ukahaba, anamchafua baba yake. Binti huyo anapaswa kuchomwa moto.+

10 “‘Kuhani mkuu miongoni mwa ndugu zake, aliyetiwa mafuta kichwani+ na kuwekwa rasmi ili avae mavazi ya kuhani,+ anapaswa kutunza nywele zake na hapaswi kurarua mavazi yake.+ 11 Hapaswi kumkaribia mtu yeyote aliyekufa;*+ hapaswi hata kujichafua kwa kumgusa baba yake au mama yake ambaye amekufa. 12 Hapaswi kuondoka mahali patakatifu wala kuchafua mahali patakatifu pa Mungu wake,+ kwa sababu ishara ya wakfu, yale mafuta ya Mungu wake yanayotumiwa kutia mafuta+ yako juu yake. Mimi ni Yehova.

13 “‘Ni lazima amwoe mwanamke ambaye ni bikira.+ 14 Hapaswi kuoa mwanamke mjane, mwanamke aliyetalikiwa, aliyenajisiwa, au kahaba; anapaswa kuoa mwanamke bikira miongoni mwa watu wake. 15 Hapaswi kuchafua uzao wake* kati ya watu wake,+ kwa sababu mimi ni Yehova, ninayemtakasa.’”

16 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 17 “Mwambie hivi Haruni: ‘Mtu yeyote wa uzao wako* katika vizazi vyako vyote ambaye ana kasoro asikaribie mahali patakatifu ili kutoa mkate wa Mungu wake. 18 Mtu yeyote mwenye kasoro hapaswi kukaribia mahali patakatifu: mtu aliye kipofu au mlemavu au mwenye majeraha usoni* au mwenye kiungo kimoja kirefu zaidi, 19 au mtu aliyevunjika mguu au aliyevunjika mkono, 20 au kibyongo au mbilikimo,* au mtu mwenye jicho lililo na kasoro au mwenye ukurutu wa ngozi au mba au mwenye mapumbu yaliyoharibika.+ 21 Mtu yeyote wa uzao wa* kuhani Haruni ambaye ana kasoro hatakaribia mahali patakatifu ili kutoa dhabihu za Yehova zinazochomwa kwa moto. Kwa sababu ana kasoro, hapaswi kupakaribia ili kutoa mkate wa Mungu wake. 22 Anaweza kula mkate wa Mungu wake kutoka kati ya vitu vitakatifu kabisa+ na kutoka kati ya vitu vitakatifu.+ 23 Hata hivyo, hapaswi kukaribia pazia+ wala madhabahu,+ kwa sababu ana kasoro mwilini; naye hapaswi kuchafua mahali pangu patakatifu,+ kwa kuwa mimi ni Yehova, ninayewatakasa.’”+

24 Basi Musa akawaambia Haruni na wanawe, na Waisraeli wote mambo hayo.

22 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Mwambie Haruni na wanawe kwamba wanapaswa kuwa waangalifu kuhusu wanavyoshughulikia* vitu vitakatifu vya Waisraeli, nao wasichafue jina langu takatifu+ kuhusu vitu wanavyotakasa kwa ajili yangu.+ Mimi ni Yehova. 3 Waambie, ‘Katika vizazi vyenu vyote, mzao wenu yeyote asiye safi atakayekaribia vitu vitakatifu ambavyo Waisraeli wanavitakasa kwa ajili yangu, mimi, Yehova, ataangamizwa kutoka mbele zangu.+ Mimi ni Yehova. 4 Mzao yeyote wa Haruni mwenye ukoma+ au anayetokwa na umajimaji+ asile vitu vitakatifu mpaka atakapokuwa safi,+ wala mtu anayemgusa mtu yeyote aliyejichafua kwa kugusa mtu aliyekufa,*+ wala mtu anayetokwa na shahawa,+ 5 wala mtu anayemgusa kiumbe asiye safi anayeishi kwenye makundi makubwa+ wala mtu anayemgusa mtu asiye safi kwa sababu yoyote ile ambaye anaweza kumchafua.+ 6 Mtu anayegusa kitu chochote kati ya vitu hivyo hatakuwa safi mpaka jioni, naye hapaswi kula kitu chochote kitakatifu, badala yake anapaswa kuoga kwenye maji.+ 7 Baada ya jua kutua, atakuwa safi, kisha anaweza kula baadhi ya vitu vitakatifu kwa sababu ni chakula chake.+ 8 Pia, hapaswi kujichafua kwa kula mnyama yeyote aliyepatikana amekufa au kiumbe yeyote aliyeraruliwa na mnyama wa mwituni.+ Mimi ni Yehova.

9 “‘Ni lazima watimize wajibu wao mbele zangu, wasije wakatenda dhambi kwa kukosa kutimiza wajibu huo na hivyo kufa kwa sababu walikuwa wakiuchafua. Mimi ni Yehova, ninayewatakasa.

10 “‘Mtu asiye na idhini* haruhusiwi kula vitu vitakatifu.+ Hakuna mgeni wa kuhani au kibarua anayepaswa kula kitu chochote kitakatifu. 11 Lakini kuhani akimnunua mtu kwa pesa zake, mtu huyo anaweza kula vitu hivyo. Vilevile watumwa waliozaliwa katika nyumba yake wanaweza kula chakula chake.+ 12 Binti ya kuhani akiolewa na mwanamume ambaye si kuhani,* hapaswi kula vitu vitakatifu vilivyotolewa mchango. 13 Lakini binti ya kuhani akiwa mjane au akitalikiwa na hana mtoto, naye arudi nyumbani kwa baba yake alikoishi kabla hajaolewa, anaweza kula kiasi fulani cha chakula cha baba yake;+ lakini mtu yeyote asiye na idhini* hapaswi kula chakula hicho.

14 “‘Mtu akila kitu kitakatifu bila kujua, ni lazima alipie kitu hicho na kuongeza sehemu ya tano ya thamani yake na kumpa kuhani.+ 15 Kwa hiyo makuhani hawapaswi kuchafua vitu vitakatifu ambavyo Waisraeli wanamtolea Yehova mchango+ 16 na hivyo kufanya Waisraeli waadhibiwe kwa sababu ya hatia ya kula vitu vyao vitakatifu; kwa maana mimi ni Yehova, ninayewatakasa.’”

17 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 18 “Waambie hivi Haruni na wanawe na Waisraeli wote: ‘Mwanamume Mwisraeli au mgeni katika Israeli anapomtolea Yehova dhabihu ya kuteketezwa+ ili kutimiza nadhiri zake au kutoa toleo la hiari,+ 19 anapaswa kutoa ng’ombe dume asiye na kasoro,+ wanakondoo dume, au mbuzi ili apate kibali. 20 Hampaswi kutoa kitu chochote chenye kasoro,+ kwa sababu hamtapata kibali mkifanya hivyo.

21 “‘Mtu akimtolea Yehova dhabihu ya ushirika+ ili kutimiza nadhiri au akiitoa ikiwa toleo la hiari, anapaswa kutoa mnyama asiye na kasoro kutoka katika mifugo yake au kundi lake, ili apate kibali. Mnyama huyo hapaswi kuwa na kasoro yoyote. 22 Hampaswi kumtoa dhabihu mnyama yeyote aliye kipofu, aliyevunjika, aliyekatwa, aliyejeruhiwa, mwenye uvimbe, vipele, au mba; hampaswi kumtolea Yehova yeyote kati ya wanyama hao au kumtolea Yehova dhabihu za aina hiyo kwenye madhabahu yake. 23 Mnaweza kumtoa ng’ombe dume au kondoo mwenye kiungo kimoja kirefu zaidi au kifupi sana kuwa toleo la hiari, lakini hatakubaliwa mkimtoa kuwa dhabihu ya nadhiri. 24 Hampaswi kumtolea Yehova mnyama mwenye mapumbu yaliyominywa au kupondwa au kung’olewa au kukatwa; hampaswi kuwatoa dhabihu wanyama wa aina hiyo katika nchi yenu. 25 Nanyi hampaswi kupokea wanyama wa aina hiyo kutoka kwa mgeni na kuwatoa kuwa dhabihu kwa* Mungu wenu, kwa sababu wana kasoro na ni walemavu. Hawatakubaliwa.’”

26 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 27 “Ng’ombe dume au mwanakondoo dume au mbuzi akizaliwa, atakaa na mama yake kwa siku saba,+ lakini kuanzia siku ya nane atapokewa kwa kibali kuwa dhabihu, dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto. 28 Lakini hampaswi kumchinja ng’ombe dume au kondoo pamoja na watoto wake siku ileile.+

29 “Mkimtolea Yehova dhabihu ya shukrani,+ mnapaswa kuitoa dhabihu hiyo ili mpate kibali chake. 30 Inapaswa kuliwa siku hiyohiyo. Hampaswi kuacha sehemu yoyote mpaka asubuhi.+ Mimi ni Yehova.

31 “Ni lazima mshike amri zangu na kuzifuata.+ Mimi ni Yehova. 32 Msilichafue jina langu takatifu,+ ni lazima nitakaswe miongoni mwa Waisraeli.+ Mimi ni Yehova, ninayewatakasa,+ 33 ninayewatoa katika nchi ya Misri ili nijithibitishe kuwa Mungu wenu.+ Mimi ni Yehova.”

23 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Waambie hivi Waisraeli: ‘Sherehe za Yehova za majira+ ambazo mnapaswa kutangaza+ ni makusanyiko matakatifu. Hizi ndizo sherehe zangu za majira:

3 “‘Mnaweza kufanya kazi kwa siku sita, lakini siku ya saba ni sabato ya pumziko kamili,+ kusanyiko takatifu. Hamtafanya kazi yoyote. Ni sabato kwa Yehova popote mnapoishi.+

4 “‘Hizi ndizo sherehe za Yehova za majira, makusanyiko matakatifu ambayo mnapaswa kutangaza katika nyakati zilizopangwa za sherehe hizo: 5 Katika siku ya 14 ya mwezi wa kwanza,+ wakati wa jioni kabla ya giza kuingia* ni Pasaka+ ya Yehova.

6 “‘Siku ya 15 ya mwezi huo ni Sherehe ya Yehova ya Mikate Isiyo na Chachu.+ Kwa siku saba mnapaswa kula mikate isiyo na chachu.+ 7 Siku ya kwanza, mtakuwa na kusanyiko takatifu.+ Hampaswi kufanya kazi yoyote ngumu. 8 Lakini kwa siku saba mtamtolea Yehova dhabihu inayochomwa kwa moto. Siku ya saba kutakuwa na kusanyiko takatifu. Hampaswi kufanya kazi yoyote ngumu.’”

9 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 10 “Waambie hivi Waisraeli: ‘Hatimaye mtakapoingia katika nchi ninayowapa na kuvuna mazao yake, ni lazima mumletee kuhani tita la mavuno yenu ya kwanza.+ 11 Naye kuhani atatikisa tita hilo mbele za Yehova kwenda mbele na nyuma ili mpate kibali. Atalitikisa siku inayofuata siku ya Sabato. 12 Siku ambayo tita hilo linatikiswa, ni lazima mumtolee Yehova dhabihu ya kuteketezwa ya mwanakondoo dume wa mwaka mmoja asiye na kasoro. 13 Mtatoa pia sehemu mbili za kumi za kipimo cha efa* ya unga laini uliochanganywa na mafuta kuwa toleo la nafaka linalochomwa kwa moto, lenye harufu inayompendeza* Yehova. Pia mtatoa robo ya hini* ya divai kuwa toleo la kinywaji. 14 Msile mkate wowote, nafaka zilizokaangwa, au nafaka zilizotoka kuvunwa, mpaka mtakapomtolea Mungu dhabihu zenu. Ni sheria ya kudumu katika vizazi vyenu vyote mahali popote mtakapoishi.

15 “‘Mnapaswa kuhesabu sabato saba kuanzia siku inayofuata siku ya Sabato, siku mnayotoa tita la toleo la kutikiswa.+ Yanapaswa kuwa majuma kamili. 16 Mtahesabu siku 50+ mpaka siku inayofuata Sabato ya saba, kisha mtamtolea Yehova toleo la nafaka iliyotoka kuvunwa.+ 17 Mnapaswa kuleta mikate miwili kutoka nyumbani ili iwe toleo la kutikiswa. Mikate hiyo inapaswa kuokwa kwa kutumia sehemu mbili za kumi za kipimo cha efa* ya unga laini. Inapaswa kuwa na chachu,+ ni mazao ya kwanza yaliyokomaa yanayotolewa kwa Yehova.+ 18 Nanyi mnapaswa kutoa mikate hiyo pamoja na wanakondoo dume saba wa mwaka mmoja wasio na kasoro, ng’ombe dume mmoja mchanga, na kondoo dume wawili.+ Watatolewa kwa Yehova wakiwa dhabihu ya kuteketezwa pamoja na toleo la nafaka na matoleo ya vinywaji, dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova. 19 Pia mnapaswa kumtoa mwanambuzi mmoja kwa ajili ya dhabihu ya dhambi+ na wanakondoo dume wawili wa mwaka mmoja kwa ajili ya dhabihu ya ushirika.+ 20 Kuhani atazitikisa dhabihu hizo kwenda mbele na nyuma pamoja na ile mikate ya mazao ya kwanza yaliyokomaa kama dhabihu ya kutikiswa mbele za Yehova, pamoja na wale wanakondoo dume wawili. Ni vitu vitakatifu vinavyotolewa kwa Yehova kwa ajili ya kuhani.+ 21 Siku hiyo mtatangaza+ na kufanya kusanyiko takatifu. Hamtafanya kazi yoyote ngumu. Ni sheria ya kudumu katika vizazi vyenu vyote mahali popote mnapoishi.

22 “‘Mnapovuna mashamba yenu, msivune kabisa ukingo wa mashamba yenu, nanyi msiokote masalio ya mavuno yenu.+ Waachieni maskini*+ na wageni.+ Mimi ni Yehova Mungu wenu.’”

23 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 24 “Waambie hivi Waisraeli: ‘Siku ya kwanza ya mwezi wa saba, mtakuwa na pumziko kamili, mtaadhimisha kusanyiko takatifu litakalotangazwa kwa mlio wa tarumbeta.+ 25 Hampaswi kufanya kazi yoyote ngumu, nanyi mtamtolea Yehova dhabihu inayochomwa kwa moto.’”

26 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 27 “Hata hivyo, siku ya kumi ya mwezi huo wa saba ni Siku ya Kufunika Dhambi.+ Mtakuwa na kusanyiko takatifu, nanyi mnapaswa kujitesa*+ na kumtolea Yehova dhabihu inayochomwa kwa moto. 28 Hampaswi kufanya kazi yoyote siku hiyo kwa sababu ni siku ya kufunika dhambi+ zenu mbele za Yehova Mungu wenu. 29 Mtu yeyote ambaye hatajitesa* siku hiyo atauawa.+ 30 Nami nitamwangamiza mtu yeyote atakayefanya kazi yoyote siku hiyo. 31 Hampaswi kufanya kazi yoyote. Ni sheria ya kudumu katika vizazi vyenu vyote mahali popote mtakapoishi. 32 Ni sabato ya pumziko kamili kwenu, nanyi mtajitesa+ siku ya tisa ya mwezi huo wakati wa jioni. Mtaadhimisha sabato kuanzia jioni hiyo mpaka jioni inayofuata.”

33 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 34 “Waambie hivi Waisraeli: ‘Siku ya 15 ya mwezi huo wa saba mtamfanyia Yehova Sherehe ya Vibanda* kwa siku saba.+ 35 Mtakuwa na kusanyiko takatifu siku ya kwanza, nanyi hampaswi kufanya kazi yoyote ngumu. 36 Kwa siku saba mtamtolea Yehova dhabihu inayochomwa kwa moto. Siku ya nane mtakuwa na kusanyiko takatifu,+ nanyi mnapaswa kumtolea Yehova dhabihu inayochomwa kwa moto. Ni kusanyiko takatifu. Hampaswi kufanya kazi yoyote ngumu.

37 “‘Hizo ndizo sherehe za Yehova za majira+ mnazopaswa kutangaza kuwa makusanyiko matakatifu+ ya kumtolea Yehova dhabihu hizi zinazochomwa moto: dhabihu ya kuteketezwa+ pamoja na toleo lake la nafaka+ na matoleo ya vinywaji+ kulingana na ratiba ya kila siku. 38 Mtazitoa pamoja na dhabihu zinazotolewa wakati wa sabato za Yehova,+ pamoja na zawadi zenu,+ dhabihu zenu za nadhiri,+ na matoleo yenu ya hiari+ ambayo mnapaswa kumtolea Yehova. 39 Hata hivyo, siku ya 15 ya mwezi wa saba, baada ya kukusanya mavuno yenu, mnapaswa kufanya sherehe ya Yehova kwa siku saba.+ Siku ya kwanza ni ya pumziko kamili na siku ya nane ni ya pumziko kamili.+ 40 Siku ya kwanza, mtachukua matunda ya miti yenu bora, matawi ya mitende,+ matawi ya miti yenye majani mengi na mierebi ya bondeni, nanyi mtashangilia+ mbele za Yehova Mungu wenu kwa siku saba.+ 41 Mtamfanyia Yehova sherehe hiyo kwa siku saba kila mwaka.+ Kwa kuwa ni sheria ya kudumu katika vizazi vyenu vyote, mnapaswa kuisherehekea katika mwezi wa saba. 42 Mtakaa katika vibanda kwa siku saba.+ Waisraeli wote watakaa katika vibanda, 43 ili vizazi vyenu vinavyokuja vijue kwamba+ niliwafanya Waisraeli wakae katika vibanda nilipowatoa nchini Misri.+ Mimi ni Yehova Mungu wenu.’”

44 Basi Musa akawaambia Waisraeli kuhusu sherehe za Yehova za majira.

24 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Waamuru Waisraeli wakuletee mafuta safi ya zeituni zilizopondwa ili taa ziwake daima.+ 3 Katika hema la mkutano, nje ya pazia lililo karibu na sanduku la ushahidi, Haruni atahakikisha kwamba taa hizo zinawaka daima kuanzia jioni mpaka asubuhi mbele za Yehova. Hiyo ni sheria ya kudumu katika vizazi vyenu vyote. 4 Haruni anapaswa kupanga taa hizo kwa utaratibu kwenye kinara cha taa+ cha dhahabu safi mbele za Yehova daima.

5 “Utachukua unga laini na kuoka mikate 12 ya mviringo. Utatumia sehemu mbili za kumi za kipimo cha efa* cha unga laini kuoka kila mkate. 6 Utaipanga mikate hiyo kwenye safu* mbili juu ya meza ya dhahabu safi mbele za Yehova,+ kila safu itakuwa na mikate sita.+ 7 Unapaswa kuweka ubani safi juu ya kila safu, na mikate hiyo itakuwa dhabihu ya kumbukumbu*+ inayochomwa kwa moto mbele za Yehova. 8 Kila siku ya Sabato, anapaswa kupanga mikate hiyo mbele za Yehova kwa ukawaida.+ Ni agano linalodumu kati yangu na Waisraeli. 9 Itakuwa ya Haruni na wanawe,+ nao wataila mahali patakatifu,+ kwa sababu ni kitu kitakatifu kabisa kwa ajili ya kuhani kutoka kwa dhabihu za Yehova zinazochomwa kwa moto; itakuwa sheria ya kudumu.”

10 Siku moja, miongoni mwa Waisraeli, mwana fulani ambaye mama yake ni Mwisraeli na baba yake ni Mmisri+ alipigana na mwanamume Mwisraeli kambini. 11 Mwana huyo wa mwanamke Mwisraeli akaanza kulikufuru lile Jina* na kulitukana.+ Basi wakamleta kwa Musa.+ Kumbe mama yake alikuwa Shelomithi, binti ya Dibri wa kabila la Dani. 12 Kwa hiyo wakamtia kifungoni mpaka walipojulishwa uamuzi wa Yehova.+

13 Kisha Yehova akamwambia Musa: 14 “Mtoeni nje ya kambi yule aliyelitukana, na wale wote waliomsikia wanapaswa kuweka mikono yao juu ya kichwa chake, kisha Waisraeli wote watampiga mawe.+ 15 Nawe utawaambia hivi Waisraeli: ‘Mtu yeyote akimtukana Mungu wake, atawajibika kwa sababu ya dhambi yake. 16 Kwa hiyo yule aliyelitukana jina la Yehova lazima auawe.+ Kwa hakika kusanyiko lote linapaswa kumpiga mawe. Mgeni anapaswa kuuawa sawasawa na mwenyeji kwa sababu ya kulitukana lile Jina.

17 “‘Mtu anayemuua mwanadamu mwenzake* lazima auawe.+ 18 Mtu yeyote anayempiga na kumuua mnyama wa kufugwa* anapaswa kulipa fidia, uhai kwa uhai.* 19 Mtu akimjeruhi mwanadamu mwenzake, basi anapaswa kutendewa jambo alilotenda.+ 20 Mfupa uliovunjika kwa mfupa uliovunjika, jicho kwa jicho, jino kwa jino, atajeruhiwa kama alivyomjeruhi mwenzake.+ 21 Mtu anayempiga na kumuua mnyama anapaswa kulipa fidia,+ lakini mtu anayempiga na kumuua mwanadamu anapaswa kuuawa.+

22 “‘Sheria itakuwa moja kwenu, iwe ni mgeni au mwenyeji,+ kwa sababu mimi ni Yehova Mungu wenu.’”

23 Basi Musa akawaambia Waisraeli mambo hayo, wakamtoa nje ya kambi yule aliyelitukana lile Jina, wakampiga mawe.+ Kwa hiyo Waisraeli wakafanya kama Yehova alivyomwamuru Musa.

25 Yehova akaendelea kumwambia Musa kwenye Mlima Sinai, 2 “Waambie hivi Waisraeli: ‘Hatimaye mtakapoingia katika nchi ninayowapa,+ nchi hiyo itashika sabato ya Yehova.+ 3 Kwa miaka sita mtapanda mbegu katika mashamba yenu, mtapunguza matawi ya mizabibu yenu, na kuvuna mazao ya nchi.+ 4 Lakini katika mwaka wa saba nchi itakuwa na pumziko kamili la sabato, sabato ya Yehova. Hampaswi kupanda mbegu wala kupunguza matawi ya mizabibu yenu. 5 Hampaswi kuvuna nafaka yoyote inayoota yenyewe baada ya mavuno, nanyi hampaswi kuchuma zabibu kutoka kwenye mizabibu yenu ambayo haijapunguzwa matawi. Ni lazima nchi iwe na mwaka wa pumziko kamili. 6 Hata hivyo, mnaweza kula mazao yanayoota nchini mwaka huo wa sabato, yaani, mtayala ninyi wenyewe, na pia watumwa wenu wa kike na wa kiume, vibarua wenu, wageni wanaoishi nanyi, 7 na pia wanyama wenu wa kufugwa na wanyama wa mwituni walio katika nchi yenu. Mnaweza kula mazao yote nchini.

8 “‘Mtahesabu miaka saba ya sabato, miaka saba mara saba, jumla ya miaka 49. 9 Kisha mtapiga pembe kwa sauti kubwa katika mwezi wa saba, siku ya kumi ya mwezi huo; katika Siku ya Kufunika Dhambi+ mnapaswa kupiga pembe katika nchi yenu yote. 10 Mtautakasa mwaka wa 50 na kutangaza uhuru kwa wakaaji wote nchini.+ Utakuwa Mwadhimisho wa Miaka 50, na kila mmoja atarudi kwenye urithi wake na kila mmoja wenu atarudi kwa familia yake.+ 11 Mwaka huo utakuwa mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50. Hamtapanda mbegu wala kuvuna nafaka iliyoota yenyewe wala kuchuma zabibu kutoka kwenye mizabibu ambayo haijapunguzwa matawi.+ 12 Kwa maana ni Mwadhimisho wa Miaka 50, ni mwaka mtakatifu kwenu. Mnaweza kula tu mazao yanayoota yenyewe nchini.+

13 “‘Katika mwaka huo wa 50, kila mmoja wenu anapaswa kurudi kwenye urithi wake.+ 14 Ukiuza au kununua chochote kutoka kwa mwenzako, usimpunje.+ 15 Bei ya unachonunua inapaswa kulingana na idadi ya miaka ambayo imepita baada ya Mwadhimisho wa Miaka 50, naye anapaswa kukuuzia kulingana na idadi ya miaka inayobaki ya mazao.+ 16 Ikiwa miaka inayobaki ni mingi, anaweza kuongeza bei, na ikiwa ni michache anapaswa kupunguza bei kwa sababu anakuuzia idadi ya mazao utakayovuna. 17 Hakuna yeyote kati yenu anayepaswa kumpunja mwenzake,+ ni lazima mmwogope Mungu wenu,+ kwa sababu mimi ni Yehova Mungu wenu.+ 18 Mkishika amri zangu na kufuata sheria zangu,* mtaishi kwa usalama nchini.+ 19 Nchi itazaa mazao yake,+ nanyi mtakula na kushiba na kuishi humo kwa usalama.+

20 “‘Iwapo mtauliza: “Tutakula nini katika mwaka wa saba tusipopanda mbegu au kuvuna mazao yetu?”+ 21 Nitaamuru baraka zangu zije juu yenu katika mwaka wa sita, nayo nchi itazaa mazao ya kutosha kwa miaka mitatu.+ 22 Nanyi mtapanda mbegu mwaka wa nane na kula mavuno ya miaka iliyotangulia mpaka mwaka wa tisa. Mtakula mavuno hayo mpaka mtakapovuna mwaka huo.

23 “‘Kwa hiyo ardhi haipaswi kuuzwa kwa muda wa kudumu,+ kwa sababu nchi ni yangu.+ Kwa maana ninyi ni wageni na wahamiaji machoni pangu.+ 24 Katika nchi yote mnayomiliki, mtakuwa na haki ya kukomboa* ardhi mliyouza.

25 “‘Ikiwa ndugu yako atakuwa maskini na hivyo alazimike kuuza sehemu fulani ya urithi wake, basi mkombozi ambaye ni mtu wake wa karibu wa ukoo atakuja na kununua sehemu iliyouzwa na ndugu yake.+ 26 Ikiwa mtu hana mkombozi lakini anapata ufanisi na kupata uwezo wa kuikomboa, 27 anapaswa kuhesabu thamani yake kulingana na miaka iliyopita tangu alipoiuza na kumrudishia yule aliyeinunua kiasi kinachobaki. Kisha atarudi kwenye urithi wake.+

28 “‘Lakini ikiwa hana uwezo wa kuikomboa sehemu aliyouza, sehemu hiyo itabaki mikononi mwa mnunuzi mpaka mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50;+ kisha atarudishiwa sehemu hiyo mwaka huo, naye atarudi kwenye urithi wake.+

29 “‘Mtu akiuza nyumba yake iliyo katika jiji lililozingirwa na ukuta, anaweza kuikomboa mwaka mmoja tangu alipoiuza; kwa mwaka mzima atakuwa na haki ya kuikomboa.+ 30 Lakini ikiwa haitakombolewa katika muda wa mwaka mzima, nyumba hiyo iliyozingirwa na ukuta itakuwa mali ya kudumu ya yule aliyeinunua katika vizazi vyake vyote. Haipaswi kurudishwa wakati wa Mwadhimisho wa Miaka 50. 31 Hata hivyo, nyumba zilizo katika vijiji ambavyo havijazingirwa na ukuta zinapaswa kuhesabiwa kama mashamba. Zinaweza kukombolewa, nazo zinapaswa kurudishwa wakati wa Mwadhimisho wa Miaka 50.

32 “‘Lakini Walawi wana haki ya kukomboa nyumba zao zilizo katika majiji yao+ wakati wowote. 33 Mlawi asipokomboa nyumba yake, nyumba hiyo iliyouzwa katika jiji la Walawi itarudishwa wakati wa Mwadhimisho wa Miaka 50,+ kwa sababu nyumba zilizo katika majiji ya Walawi ni urithi wao miongoni mwa Waisraeli.+ 34 Isitoshe, malisho+ yanayozunguka majiji yao hayapaswi kuuzwa, kwa sababu ni urithi wao wa kudumu.

35 “‘Ikiwa ndugu yako aliye karibu nawe amekuwa maskini na hawezi kujiruzuku, unapaswa kumsaidia,+ kama ambavyo ungemsaidia mgeni na pia mhamiaji,+ ili aendelee kuwa hai kama wewe. 36 Usimtoze riba au kujipatia faida kutoka kwake.+ Ni lazima umwogope Mungu wako,+ na ndugu yako ataendelea kuwa hai kama wewe. 37 Usimkopeshe pesa kwa riba+ au kumpa chakula ili upate faida. 38 Mimi ni Yehova Mungu wenu, niliyewatoa nchini Misri+ ili kuwapa nchi ya Kanaani, ili nijithibitishe kuwa Mungu wenu.+

39 “‘Ikiwa ndugu yako anayeishi karibu nawe amelazimika kujiuza kwako+ kwa sababu amekuwa maskini, usimlazimishe akutumikie kama mtumwa.+ 40 Unapaswa kumtendea kama kibarua,+ kama mhamiaji. Atakutumikia mpaka wakati wa Mwadhimisho wa Miaka 50. 41 Kisha atakuacha, yeye na watoto* wake, na kurudi kwa watu wake wa ukoo. Anapaswa kurudi kwenye urithi wa mababu zake.+ 42 Kwa maana wao ni watumwa wangu niliowatoa nchini Misri.+ Hawapaswi kujiuza kama mtumwa anavyouzwa. 43 Usimtendee kwa ukatili,+ ni lazima umwogope Mungu wako.+ 44 Utawachukua watumwa wa kike na wa kiume kutoka katika mataifa jirani, unaweza kumnunua mtumwa wa kiume au wa kike kutoka katika mataifa hayo. 45 Pia unaweza kununua watumwa kutoka miongoni mwa wana wa wageni wanaoishi nawe+ na kutoka kati ya watu wa familia zao waliozaliwa katika nchi yenu, nao watakuwa mali yako. 46 Unaweza kuwarithisha kwa wana wako ili wawe mali yao ya kudumu. Unaweza kuwatumia watumwa hao kama wafanyakazi, lakini usiwatendee ndugu zako Waisraeli kwa ukatili.+

47 “‘Lakini ikiwa mgeni au mhamiaji miongoni mwenu amekuwa tajiri na ndugu yako amekuwa maskini kando yake na hivyo analazimika kujiuza kwa mgeni au mhamiaji huyo anayeishi miongoni mwenu, au kwa mtu wa ukoo wa mgeni huyo, 48 ndugu yako ambaye amejiuza ataendelea kuwa na haki ya ukombozi hata baada ya kujiuza. Mmoja wa ndugu zake anaweza kumkomboa,+ 49 au anaweza kukombolewa na ndugu ya baba yake au binamu yake, au na mtu yeyote wa karibu wa ukoo,* yaani, mtu wa familia yake.

“‘Au anaweza kujikomboa mwenyewe akipata utajiri.+ 50 Yeye pamoja na mtu aliyemnunua watahesabu idadi ya miaka tangu mwaka aliojiuza mpaka mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50,+ na bei ya kukombolewa kwake itahesabiwa kulingana na idadi hiyo ya miaka.+ Muda aliofanya kazi utapimwa kama muda wa mtu anayefanya kazi ya kibarua.+ 51 Ikiwa miaka inayobaki ni mingi, anapaswa kulipa bei yake ya ukombozi kulingana na miaka inayobaki. 52 Lakini ikiwa ni miaka michache tu inayobaki kabla ya mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50, anapaswa kuhesabu mwenyewe bei yake ya ukombozi na kulipa kulingana na miaka inayobaki. 53 Ataendelea kumtumikia kama kibarua mwaka baada ya mwaka; mnapaswa kuhakikisha kwamba yule aliyemnunua hamtendei kwa ukatili.+ 54 Hata hivyo, ikiwa hawezi kujinunua kulingana na masharti hayo, ataachiliwa huru pamoja na watoto* wake wakati wa Mwadhimisho wa Miaka 50.+

55 “‘Kwa maana Waisraeli ni watumwa wangu mwenyewe. Ni watumwa wangu niliowatoa nchini Misri.+ Mimi ni Yehova Mungu wenu.

26 “‘Msijitengenezee miungu ya ubatili+ wala sanamu ya kuchongwa+ au nguzo takatifu, nanyi msichonge sanamu ya mawe+ katika nchi yenu na kuiinamia;+ kwa maana mimi ni Yehova Mungu wenu. 2 Mnapaswa kushika sabato zangu na kuheshimu* mahali pangu patakatifu. Mimi ni Yehova.

3 “‘Mkiendelea kufuata sheria zangu na kushika amri zangu na kuzitekeleza,+ 4 nitawaletea mvua katika majira yanayofaa,+ nayo nchi itazaa kwa wingi,+ na miti ya matunda itazaa matunda mengi. 5 Majira yenu ya kupura nafaka yataendelea mpaka wakati wa kuvuna zabibu, na wakati wa kuvuna zabibu utaendelea mpaka wakati wa kupanda; nanyi mtakula mkate na kushiba na kuishi kwa usalama katika nchi yenu.+ 6 Nitaleta amani nchini,+ nanyi mtalala na hakuna yeyote atakayewaogopesha;+ nami nitawaondoa nchini wanyama wote wakali wa mwituni, na hakuna mtu yeyote atakayewashambulia kwa upanga katika nchi yenu. 7 Nanyi hakika mtawakimbiza maadui wenu na kuwaua kwa upanga. 8 Watu watano kati yenu watawakimbiza maadui 100, na 100 watawakimbiza 10,000; mtawaua maadui wenu kwa upanga.+

9 “‘Nitawabariki* na kuwafanya mzaane na kuongezeka,+ nami nitatimiza agano nililofanya pamoja nanyi.+ 10 Wakati wa mavuno mtakuwa bado mnakula mavuno ya zamani ya mwaka uliotangulia, mtahitaji kuondoa mavuno hayo ya zamani ili mpate nafasi ya mavuno mapya. 11 Nami nitaweka hema langu la ibada kati yenu,+ nami sitawakataa. 12 Nitatembea kati yenu na kuwa Mungu wenu,+ nanyi mtakuwa watu wangu.+ 13 Mimi ni Yehova Mungu wenu, niliyewatoa katika nchi ya Misri ili msiendelee kuwa watumwa wao, nami nikavunja nira yenu na kuwafanya mtembee vichwa vyenu vikiwa vimeinuliwa.*

14 “‘Lakini msiponisikiliza au kushika amri hizo zote,+ 15 mkikataa masharti yangu,+ mkichukia sheria zangu,* na kuvunja agano langu kwa kuacha kushika amri zangu zote,+ 16 basi, mimi nitawatendea mambo haya: nitawaadhibu kwa taabu, kwa kifua kikuu na homa kali, na kufanya macho yenu yadhoofike na uhai wenu uzorote.* Mtapanda mbegu zenu bure, kwa maana maadui wenu watazila.+ 17 Nitawakataa,* nanyi mtashindwa na maadui wenu;+ na wale wanaowachukia ninyi watawakanyaga-kanyaga,+ nanyi mtakimbia bila kukimbizwa na mtu.+

18 “‘Hata mambo hayo yasipowafanya mnisikilize, nitalazimika kuwaadhibu mara saba zaidi kwa sababu ya dhambi zenu. 19 Nitakivunja kiburi chenu cha ukaidi na kufanya mbingu zenu ziwe kama chuma+ na nchi yenu kama shaba. 20 Mtapoteza nguvu zenu bure, kwa maana nchi yenu haitazaa mazao yake,+ na miti iliyo nchini haitazaa matunda.

21 “‘Lakini mkiendelea kunipinga na kukataa kunisikiliza, ndipo mimi nitalazimika kuwapiga mara saba zaidi, kulingana na dhambi zenu. 22 Nitaleta wanyama wa mwituni kati yenu,+ nao watawaua watoto wenu,+ wataangamiza mifugo yenu na kupunguza idadi yenu, na barabara zenu hazitakuwa na watu.+

23 “‘Msipokubali nidhamu yangu+ licha ya mambo hayo, nanyi kwa ushupavu mtembee kwa kunipinga, 24 basi mimi pia nitawapinga, nami mwenyewe nitawapiga mara saba kwa sababu ya dhambi zenu. 25 Nitaleta dhidi yenu upanga unaolipiza kisasi kwa sababu ya kulivunja agano langu.+ Hata mkikusanyika katika majiji yenu, nitaleta magonjwa katikati yenu+ na kuwatia mikononi mwa adui.+ 26 Nitakapoharibu hifadhi yenu ya* mikate,+ wanawake kumi wataoka mikate kwenye jiko moja tu na kuwapimia mikate kwa mizani;+ nanyi mtakula lakini hamtashiba.+

27 “‘Na ikiwa hamtanisikiliza, nanyi mkinipinga kwa ushupavu licha ya mambo hayo, 28 nitazidisha upinzani wangu dhidi yenu,+ na mimi mwenyewe nitawaadhibu mara saba kwa sababu ya dhambi zenu. 29 Basi mtalazimika kula nyama ya wana wenu na nyama ya mabinti wenu.+ 30 Nitaharibu mahali penu patakatifu palipo juu+ na kuvikatakata vinara vyenu vya uvumba, nami nitarundika mizoga yenu juu ya mizoga ya sanamu zenu zenye kuchukiza,*+ nami nitawachukia na kuwaacha.+ 31 Nitayaangamiza majiji yenu kwa upanga+ na kuharibu mahali penu patakatifu, nami sitasikia harufu inayopendeza* ya dhabihu zenu. 32 Mimi mwenyewe nitaifanya nchi yenu iwe ukiwa,+ na maadui wenu watakaoishi humo watashangazwa na hali yake.+ 33 Nitawatawanya miongoni mwa mataifa,+ nitachomoa upanga nanyi mtakimbizwa;+ na nchi yenu itaharibiwa, na majiji yenu yatabaki ukiwa.+

34 “‘Wakati huo nchi italipa sabato zake siku zote itakapokuwa ukiwa, mtakapokuwa katika nchi ya maadui wenu. Wakati huo nchi itapumzika,* kwa maana ni lazima ilipe sabato zake.+ 35 Siku zote itakapokuwa ukiwa itapumzika, kwa sababu haikupumzika wakati wa sabato zenu mlipokuwa mkiishi humo.

36 “‘Nitajaza hisia ya kukata tamaa mioyoni mwa wale watakaobaki+ katika nchi za maadui wao; na sauti ya jani linalopeperushwa na upepo itawafanya wakimbie, nao watakimbia kama mtu anayeukimbia upanga na kuanguka bila kukimbizwa na yeyote.+ 37 Watajikwaa na kuangukiana kama watu wanaokimbia upanga, hata ingawa hakuna anayewakimbiza. Hamtaweza kuwashinda maadui wenu.+ 38 Mtaangamia miongoni mwa mataifa,+ na nchi ya maadui wenu itawala. 39 Wale watakaobaki wataachwa waoze katika nchi za maadui wenu+ kwa sababu ya dhambi zenu. Naam, wataozea huko kwa sababu ya dhambi za baba zao.+ 40 Kisha wataungama dhambi zao,+ wataungama pia dhambi na ukosefu wa uaminifu wa baba zao, nao watakiri kwamba hawakuwa waaminifu waliponipinga mimi.+ 41 Basi nikalazimika kuwapinga+ kwa kuwapeleka katika nchi ya maadui wao.+

“‘Nilifanya hivyo ili mioyo yao mikaidi* inyenyekee,+ na ili walipie dhambi zao. 42 Nitakumbuka agano langu na Yakobo,+ na agano langu na Isaka,+ na pia agano langu na Abrahamu,+ nami nitaikumbuka nchi yao. 43 Walipokuwa wameiacha nchi yao, ilikuwa ikilipa sabato zake+ na kukaa ukiwa bila mtu yeyote, nao walikuwa wakilipia dhambi zao, kwa sababu walikataa amri zangu na kuchukia sheria zangu.+ 44 Lakini licha ya hayo yote, wakiwa katika nchi ya maadui wao, sitawakataa kabisa+ wala sitawatupa na kuwaangamiza kabisa na hivyo kulivunja agano nililofanya+ pamoja nao; kwa maana mimi ni Yehova Mungu wao. 45 Kwa ajili yao nitalikumbuka agano nililofanya na mababu zao+ niliowatoa nchini Misri mataifa yakishuhudia,+ ili nijithibitishe mwenyewe kuwa Mungu wao. Mimi ni Yehova.’”

46 Hayo ndiyo masharti, amri, na sheria ambazo Yehova aliwapa Waisraeli kwenye Mlima Sinai kupitia Musa.+

27 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Waambie hivi Waisraeli: ‘Mtu akiweka nadhiri ya pekee+ ya kumtolea Yehova thamani inayokadiriwa ya mtu,* 3 thamani ya mwanamume mwenye umri wa kuanzia miaka 20 mpaka miaka 60 itakadiriwa kuwa shekeli 50* za fedha kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu.* 4 Lakini ikiwa ni mwanamke, thamani yake itakadiriwa kuwa shekeli 30. 5 Ikiwa mtu ana umri wa kuanzia miaka 5 mpaka miaka 20, thamani ya mwanamume itakadiriwa kuwa shekeli 20 na ya mwanamke shekeli 10. 6 Ikiwa mtu ana umri wa kuanzia mwezi mmoja mpaka miaka mitano, thamani ya mtoto wa kiume itakadiriwa kuwa shekeli tano za fedha na ya mtoto wa kike shekeli tatu za fedha.

7 “‘Ikiwa mtu ana umri wa miaka 60 na zaidi, thamani ya mwanamume itakadiriwa kuwa shekeli 15 na ya mwanamke shekeli 10. 8 Lakini ikiwa mtu anayeweka nadhiri hawezi kulipa thamani iliyokadiriwa kwa sababu ni maskini sana,+ mtu huyo atasimama mbele ya kuhani, naye kuhani atakadiria thamani yake. Atakadiria thamani yake kulingana na kiasi ambacho mtu anayeweka nadhiri anaweza kulipa.+

9 “‘Ikiwa nadhiri inahusisha mnyama anayestahili kutolewa kwa Yehova, basi chochote kinachotolewa kwa Yehova kitakuwa kitu kitakatifu. 10 Hawezi kumbadilisha mnyama aliyemweka kuwa nadhiri, yaani, achukue mnyama mzuri na kumtoa mbaya, au achukue mbaya na kumtoa mzuri. Lakini akimbadilisha mnyama huyo na mwingine, wanyama wote wawili watakuwa watakatifu. 11 Ikiwa ni mnyama asiye safi+ ambaye hawezi kutolewa kwa Yehova, mnyama huyo atapelekwa mbele ya kuhani. 12 Halafu kuhani atakadiria thamani yake, ataamua ikiwa ni mzuri au mbaya. Thamani itakayokadiriwa na kuhani ndiyo itakayokuwa thamani ya mnyama huyo. 13 Lakini ikiwa mtu huyo anataka kumnunua tena mnyama huyo, ni lazima alipe thamani ya mnyama huyo pamoja na sehemu ya tano ya thamani iliyokadiriwa.+

14 “‘Sasa ikiwa mtu ataitakasa nyumba yake ili iwe takatifu kwa Yehova, kuhani atakadiria thamani ya nyumba hiyo, iwapo ni nzuri au ni mbaya. Thamani itakayokadiriwa na kuhani ndiyo itakayokuwa bei yake.+ 15 Lakini ikiwa mtu anayetakasa nyumba yake anataka kuinunua tena, ni lazima alipe thamani iliyokadiriwa pamoja na sehemu ya tano ya thamani hiyo, kisha itakuwa yake.

16 “‘Mtu akitakasa sehemu fulani ya shamba lake ili iwe ya Yehova, thamani yake itakadiriwa kulingana na kiasi cha mbegu zinazohitajika kupandwa: thamani ya homeri moja* ya mbegu za shayiri itakuwa shekeli 50 za fedha. 17 Ikiwa atalitakasa shamba lake kuanzia mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50,+ thamani yake itabaki kama ilivyokadiriwa. 18 Ikiwa atalitakasa shamba lake baada ya mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50, kuhani atakadiria bei kulingana na miaka inayobaki kabla ya mwadhimisho unaofuata wa miaka 50, naye atapunguza thamani iliyokadiriwa.+ 19 Lakini ikiwa yule aliyelitakasa shamba hilo anataka kulinunua tena, ni lazima alipe thamani yake pamoja na sehemu ya tano ya thamani iliyokadiriwa, kisha litakuwa lake. 20 Asipolinunua, kisha mtu mwingine auziwe shamba hilo, haliwezi kununuliwa tena. 21 Yule aliyenunua shamba hilo akiliacha wakati wa Mwadhimisho wa Miaka 50, litakuwa kitu kitakatifu kwa Yehova, shamba lililotolewa kwa ajili yake. Litakuwa mali ya makuhani.+

22 “‘Mtu akitakasa shamba alilonunua ambalo si sehemu ya urithi wake na kulitoa liwe mali ya Yehova,+ 23 kuhani atamhesabia thamani ya shamba hilo kufikia mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50, na mtu huyo atalipa siku hiyo thamani iliyokadiriwa.+ Ni kitu kitakatifu kwa Yehova. 24 Katika mwaka wa Mwadhimisho wa Miaka 50, shamba litarudishwa kwa yule aliyeliuza, kwa mtu ambaye shamba hilo ni mali yake.+

25 “‘Thamani ya kila kitu itakadiriwa kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu. Shekeli moja ni sawa na gera 20.*

26 “‘Hata hivyo, hakuna mtu yeyote anayepaswa kumtakasa mzaliwa wa kwanza wa wanyama, kwa sababu mzaliwa wa kwanza ni wa Yehova.+ Awe ni ng’ombe dume au kondoo, tayari ni wa Yehova.+ 27 Ikiwa mtu anamkomboa mnyama asiye safi kulingana na thamani iliyokadiriwa, anapaswa kulipa thamani ya mnyama huyo pamoja na sehemu ya tano ya thamani hiyo.+ Lakini asipomkomboa, mnyama huyo atauzwa kulingana na thamani iliyokadiriwa.

28 “‘Lakini kitu chochote ambacho mtu anamtolea Yehova bila masharti,* iwe ni mwanadamu au mnyama au shamba lake, hakiwezi kuuzwa au kununuliwa tena. Kitu chochote kilichowekwa wakfu ni kitakatifu kabisa kwa Yehova.+ 29 Zaidi ya hayo, mtu yeyote aliyehukumiwa na kutengwa ili aangamizwe hawezi kukombolewa.+ Ni lazima auawe.+

30 “‘Kila sehemu ya kumi+ ya mazao ya ardhi au matunda ni mali ya Yehova. Sehemu hiyo ni takatifu kwa Yehova. 31 Ikiwa mtu anataka kununua tena sehemu yoyote ya kumi aliyotoa, anapaswa kulipa thamani yake pamoja na sehemu ya tano ya thamani hiyo. 32 Kila sehemu ya kumi ya mifugo na ya kundi, yaani, kila mnyama wa kumi anayepita* chini ya fimbo ya mchungaji atakuwa mtakatifu kwa Yehova. 33 Mtu huyo hapaswi kuchunguza ikiwa mnyama huyo ni mzuri au mbaya, wala hapaswi kumbadilisha na mwingine. Ikiwa atambadilisha na mwingine, basi wanyama wote wawili watakuwa watakatifu.+ Hawawezi kununuliwa tena.’”

34 Hizo ndizo sheria ambazo Yehova alimpa Musa kwenye Mlima Sinai ili awape Waisraeli.+

Tnn., “wana wa Israeli.”

Au “inayomtuliza.”

Au “inayomtuliza.”

Au “majivu yenye mafuta,” yaani, majivu yaliyojaa mafuta ya dhabihu.

Au “inayomtuliza.”

Au “ikiwa sehemu ya ukumbusho (uwakilishi) wake.”

Au “inayomtuliza.”

Au “ikiwa sehemu ya ukumbusho (uwakilishi) wake.”

Au “inayomtuliza.”

Au “inayotuliza.”

Au “ikiwa sehemu ya ukumbusho (uwakilishi) wake.”

Au “dhabihu ya matoleo ya amani.”

Au “inayomtuliza.”

Tnn., “mkate,” yaani, sehemu ya Mungu ya dhabihu ya ushirika.

Tnn., “mkate,” yaani, sehemu ya Mungu ya dhabihu ya ushirika.

Au “inayotuliza.”

Au “majivu yenye mafuta,” yaani, majivu yaliyojaa mafuta ya dhabihu.

Au “inayomtuliza.”

Tnn., “amesikia laana (kiapo).” Labda anasikia tangazo kuhusu kosa lililofanywa na laana itakayompata mkosaji au shahidi yeyote anayekataa kutoa ushahidi.

Inaonekana mtu huyo hatimizi kiapo chake.

Sehemu ya kumi ya efa ilikuwa sawa na lita 2.2 au kilogramu 1.3 hivi. Angalia Nyongeza B14.

Au “ukiwa sehemu ya ukumbusho (uwakilishi) wake.”

Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.

Au “shekeli takatifu.”

Au “suruali ya ndani.”

Au “majivu yenye mafuta,” yaani, majivu yaliyojaa mafuta ya dhabihu.

Au “inayotuliza.”

Au “ukiwa sehemu ya ukumbusho (uwakilishi) wake.”

Sehemu ya kumi ya efa ilikuwa sawa na lita 2.2 au kilogramu 1.3 hivi. Angalia Nyongeza B14.

Au “inayomtuliza.”

Au “lile taji takatifu.”

Au “inayotuliza.”

Au “kutuliza.”

Au “masharti yote ambayo.”

Au “tai mla mizoga.”

Au “tai mla mizoga.”

Au “Kila mdudu.”

Au “nyenje.”

Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “ukoma” lina maana pana na linaweza kutia ndani magonjwa mbalimbali ya ngozi yanayoambukiza. Linaweza pia kutia ndani maambukizi fulani yaliyopatikana kwenye nguo na nyumba.

Au “ambukizo hilo limeenea.”

Au “mara ya pili.”

Yaani, hapaswi kumtenga kwa uchunguzi zaidi.

Au “hawezi kuwaambukiza wengine.”

Sehemu tatu za kumi za efa zilikuwa sawa na lita 6.6 au kilogramu 3.9 hivi. Angalia Nyongeza B14.

Logi ilikuwa sawa na lita 0.3. Angalia Nyongeza B14.

Sehemu ya kumi ya efa ilikuwa sawa na lita 2.2 au kilogramu 1.3 hivi. Angalia Nyongeza B14.

Tnn., “yenye dhambi.”

Tnn., “yenye dhambi.”

Tnn., “mwili wake.”

Au “suruali ya ndani.”

Au “uchi wake.”

Huenda neno hili linamaanisha “Mbuzi Anayetoweka.”

Au “aliye tayari.”

Kwa ujumla inaeleweka kwamba “kujitesa” kunamaanisha kujinyima kwa njia mbalimbali, kutia ndani kufunga.

Au “kuitesa nafsi yenu.”

Tnn., “ambaye mkono wake utajazwa.”

Tnn., “Amemwaga damu.”

Au “inayomtuliza.”

Tnn., “kwa wale mbuzi.”

Tnn., “nitaukaza uso wangu dhidi ya.”

Au “nafsi ya kiumbe imo.”

Au “nafsi ya.”

Au “nafsi imo.”

Tnn., “maamuzi yangu ya hukumu.”

Tnn., “maamuzi yangu ya hukumu.”

Tnn., “kufunua uchi wake.”

Tnn., “Ni uchi wa baba yako.”

Tnn., “Usifunue uchi wa.”

Tnn., “ni uchi wa ndugu yako.”

Au “ni mwenendo wa aibu; mwenendo mchafu uliopotoka.”

Au “rafiki yako.”

Tnn., “maamuzi yangu ya hukumu.”

Tnn., “kumwogopa.”

Au “wanaoteseka.”

Au “Usimlaani.”

Tnn., “damu ya.”

Tnn., “kuwa kama magovi yake.”

Tnn., “Kwa miaka mitatu hayajatahiriwa.”

Au “Msipunguze; Msikate.”

Au “kwa ajili ya nafsi iliyokufa.” Neno la Kiebrania neʹphesh katika andiko hili linamaanisha mtu aliyekufa.

Tnn., “kuogopa.”

Tnn., “kipimo sahihi cha efa.” Angalia Nyongeza B14.

Tnn., “kipimo sahihi cha hini.” Angalia Nyongeza B14.

Tnn., “maamuzi yangu yote ya hukumu.”

Tnn., “nitaukaza uso wangu dhidi ya.”

Tnn., “nitaukaza uso wangu dhidi ya.”

Au “anayemlaani.”

Tnn., “damu yake itakuwa juu ya kichwa chake.”

Tnn., “amefunua uchi wa baba yake.”

Tnn., “Damu yao itakuwa juu ya vichwa vyao.”

Tnn., “Damu yao itakuwa juu ya vichwa vyao.”

Tnn., “Damu yao itakuwa juu ya vichwa vyao.”

Au “ni mwenendo wa aibu; mwenendo mchafu uliopotoka.”

Tnn., “Damu yao itakuwa juu ya vichwa vyao.”

Tnn., “Amefunua uchi wa dada yake.

Tnn., “amefunua uchi wa.”

Tnn., “Amefunua uchi wa ndugu yake.”

Au “ana roho ya ubashiri.”

Tnn., “Damu yao itakuwa juu ya vichwa vyao.”

Au “kuigusa nafsi iliyokufa.”

Au “chakula cha,” yaani, dhabihu.

Au “kuikaribia nafsi yoyote iliyokufa.”

Tnn., “mbegu yake.”

Tnn., “mbegu yako.”

Tnn., “pua iliyokatika.”

Au labda, “aliyekonda na kudhoofika.”

Tnn., “mbegu ya.”

Tnn., “kuhusu jinsi wanavyopaswa kujitenga na.”

Au “nafsi iliyokufa.”

Tnn., “Mgeni,” yaani, mtu ambaye si wa familia ya Haruni.

Au “ni mgeni.”

Tnn., “mgeni yeyote,” yaani, mtu ambaye si wa familia ya Haruni.

Tnn., “mkate wa.”

Tnn., “katikati ya zile jioni mbili.”

Sehemu mbili za kumi za efa zilikuwa sawa na lita 4.4 au kilogramu 2.6 hivi. Angalia Nyongeza B14.

Au “inayomtuliza.”

Hini ilikuwa sawa na lita 3.67. Angalia Nyongeza B14.

Sehemu mbili za kumi za efa zilikuwa sawa na lita 4.4 au kilogramu 2.6 hivi. Angalia Nyongeza B14.

Au “inayomtuliza.”

Au “wanaoteseka.”

Kwa ujumla inaeleweka kwamba “kujitesa” kunamaanisha kujinyima kwa njia mbalimbali, kutia ndani kufunga.

Au labda, “hatafunga.”

Au “Vibanda vya Muda.”

Sehemu mbili za kumi za efa zilikuwa sawa na lita 4.4 au kilogramu 2.6 hivi. Angalia Nyongeza B14.

Au “tabaka.”

Au “itakuwa sehemu ya ukumbusho (uwakilishi) wake.”

Yaani, jina Yehova, kulingana na mstari wa 15 na 16.

Au “anayeua nafsi yoyote ya mwanadamu.”

Au “anayepiga na kuua nafsi ya mnyama.”

Au “nafsi kwa nafsi.”

Tnn., “maamuzi yangu ya hukumu.”

Au “kununua tena.”

Tnn., “wana.”

Au “mwenye uhusiano wa damu naye.”

Tnn., “wana.”

Au “kuogopa.”

Au “Nitawakazia fikira.”

Tnn., “mtembee wima.”

Tnn., “maamuzi yangu ya hukumu.”

Au “nafsi yenu izorote.”

Tnn., “Nitaukaza uso wangu dhidi yenu.”

Tnn., “fito zenu za.” Labda ni fito zilizotumiwa kuhifadhia mikate.

Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.

Au “inayotuliza.”

Au “itashika sabato.”

Tnn., “mioyo yao ambayo haijatahiriwa.”

Au “nafsi.”

Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.

Au “shekeli takatifu.”

Homeri ni kipimo sawa na lita 220. Angalia Nyongeza B14.

Gera moja ilikuwa na uzito wa gramu 0.57. Angalia Nyongeza B14.

Au “ili kiangamizwe.”

Au “kichwa cha kumi kinachopita.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki