KUTOKA
1 Sasa haya ndiyo majina ya wana wa Israeli walioingia Misri pamoja na Yakobo, kila mwanamume aliyekuja na watu wa nyumba yake:+ 2 Rubeni, Simeoni, Lawi, na Yuda;+ 3 Isakari, Zabuloni, na Benjamini; 4 Dani na Naftali; Gadi na Asheri.+ 5 Na wazao wote wa Yakobo* walikuwa 70, lakini tayari Yosefu alikuwa Misri.+ 6 Mwishowe Yosefu akafa,+ na pia ndugu zake wote na kizazi hicho chote. 7 Na Waisraeli* wakazaana na kuanza kuongezeka sana, nao wakazidi kuwa wengi na kuwa na nguvu isivyo kawaida, hivi kwamba wakajaa nchini.+
8 Baada ya muda mfalme mpya ambaye hakumjua Yosefu akaanza kutawala Misri. 9 Akawaambia watu wake: “Tazameni! Waisraeli ni wengi zaidi na wenye nguvu kuliko sisi.+ 10 Acheni tushughulike nao kwa akili. La sivyo, wataendelea kuongezeka, na vita vikitokea, wataungana na maadui wetu na kupigana nasi na kuondoka nchini.”
11 Basi wakaweka wasimamizi wa kazi za utumwa* ili wawatumikishe na kuwakandamiza kwa kazi ngumu,+ nao wakamjengea Farao majiji yenye maghala, yaani, Pithomu na Raamsesi.+ 12 Lakini kadiri walivyozidi kuwakandamiza, ndivyo walivyozidi kuongezeka na ndivyo walivyozidi kuenea kotekote, kwa hiyo wakaogopa sana na kuchukizwa na Waisraeli.+ 13 Kwa hiyo, Wamisri wakawalazimisha Waisraeli kuwa watumwa na kuwatesa kikatili.+ 14 Wakafanya maisha yao yawe machungu kwa kazi ngumu ya kutengeneza saruji ya udongo wa mfinyanzi na matofali na katika kila aina ya utumwa shambani. Naam, waliwalazimisha wafanye kazi ngumu chini ya hali ngumu sana katika kila aina ya utumwa.+
15 Baadaye mfalme wa Misri akazungumza na wakunga Waebrania walioitwa Shifra na Pua, 16 akawaambia: “Mnapowasaidia wanawake Waebrania kuzaa,+ wanapokuwa kwenye kiti cha kuzalia, mnapaswa kumuua mtoto huyo ikiwa ni wa kiume; lakini ikiwa ni wa kike, mwacheni aishi.” 17 Hata hivyo, wakunga hao walimwogopa Mungu wa kweli, kwa hiyo hawakufanya kama walivyoambiwa na mfalme wa Misri. Badala yake, waliwaacha watoto wa kiume waishi.+ 18 Baada ya muda mfalme wa Misri akawaita wakunga hao na kuwauliza: “Kwa nini mmewaacha watoto wa kiume waishi?” 19 Wakunga hao wakamjibu Farao: “Wanawake Waebrania si kama wanawake Wamisri. Wana nguvu nao huzaa kabla mkunga hajafika.”
20 Kwa hiyo Mungu akawatendea mema wakunga hao, na Waisraeli wakazidi kuongezeka na kuwa wenye nguvu sana. 21 Na kwa sababu wakunga hao walimwogopa Mungu wa kweli, baadaye aliwapa familia. 22 Hatimaye Farao akawaamuru hivi watu wake wote: “Mnapaswa kumtupa kwenye Mto Nile kila mtoto mchanga wa kiume anayezaliwa na Waebrania, lakini mtamwacha hai kila mtoto wa kike.”+
2 Karibu na wakati huo, mwanamume fulani wa nyumba ya Lawi alimwoa binti ya Lawi.+ 2 Mwanamke huyo akapata mimba na kuzaa mwana. Alipoona kwamba mwana huyo ana sura yenye kupendeza sana, alimficha kwa miezi mitatu.+ 3 Aliposhindwa kuendelea kumficha,+ alichukua kikapu cha mafunjo* na kukipaka lami na bereu, akamweka mtoto huyo ndani yake na kukiweka kati ya matete kando ya Mto Nile. 4 Lakini dada ya mtoto huyo+ akasimama mbali kidogo ili aone yatakayompata ndugu yake.
5 Binti ya Farao aliposhuka kwenye Mto Nile ili kuoga, watumishi wake wa kike walikuwa wakitembeatembea kando ya Mto Nile. Binti ya Farao akaona kikapu hicho kati ya matete. Mara moja akamtuma kijakazi wake akilete.+ 6 Alipokifungua, alimwona mwana huyo akilia. Akamhurumia, lakini akasema: “Huyu ni mtoto wa Waebrania.” 7 Kisha dada ya mtoto huyo akamuuliza binti ya Farao: “Je, niende nikamwite mwanamke mlezi Mwebrania akunyonyeshee mtoto huyu?” 8 Binti ya Farao akamwambia: “Nenda!” Msichana huyo akaenda mara moja na kumwita mama ya mtoto huyo.+ 9 Kisha binti ya Farao akamwambia: “Mchukue mtoto huyu uninyonyeshee, nami nitakulipa.” Basi mwanamke huyo akamchukua na kumnyonyesha. 10 Mtoto huyo alipokuwa mkubwa kidogo, akamleta kwa binti ya Farao, naye akawa mwanawe.+ Akampa jina Musa* na kusema: “Ni kwa sababu nimemtoa katika maji.”+
11 Siku hizo, baada ya Musa kuwa mtu mzima,* alitoka kwenda kwa ndugu zake ili kuona mizigo waliyokuwa wakibeba,+ akamwona Mmisri akimpiga Mwebrania, mmoja wa ndugu zake. 12 Kwa hiyo Musa akatazama huku na kule, na alipoona kwamba hakuna yeyote, akamuua Mmisri huyo na kumficha mchangani.+
13 Lakini Musa alitoka siku iliyofuata, akawaona wanaume wawili Waebrania wakipigana. Basi akamuuliza yule aliyekosea: “Kwa nini unampiga mwenzako?”+ 14 Akasema: “Ni nani aliyekuweka kuwa mkuu na mwamuzi wetu? Je, unapanga kuniua kama ulivyomuua yule Mmisri?”+ Basi Musa akaogopa na kusema moyoni: “Bila shaka jambo hilo limejulikana!”
15 Kisha Farao akasikia habari hizo, naye akajaribu kumuua Musa; lakini Musa akamkimbia Farao na kwenda kuishi katika nchi ya Midiani;+ alipofika huko akaketi kando ya kisima. 16 Sasa kuhani wa Midiani+ alikuwa na mabinti saba, nao wakaja kuteka maji na kujaza vyombo vya kunyweshea kondoo wa baba yao. 17 Lakini kama kawaida, wachungaji walikuja na kuwafukuza mabinti hao. Kwa hiyo Musa akainuka, akawasaidia* wanawake hao, na kuwanywesha kondoo wao. 18 Walipofika nyumbani kwa Reueli*+ baba yao, akawauliza kwa mshangao: “Mbona mmerudi upesi sana leo?” 19 Wakamjibu: “Mmisri fulani+ alituokoa kutoka mikononi mwa wachungaji, na hata alitutekea maji na kuwanywesha kondoo.” 20 Reueli akawaambia mabinti zake: “Lakini yuko wapi? Kwa nini hamkuja naye? Mwiteni, ili ale chakula pamoja nasi.” 21 Baada ya hayo Musa akakubali kuishi na mtu huyo, naye akampa Musa binti yake aliyeitwa Sipora+ ili amwoe. 22 Baadaye Sipora akazaa mwana, naye Musa akamwita mwana huyo Gershomu,*+ kwa sababu alisema: “Nimekuwa mkaaji mgeni katika nchi ya kigeni.”+
23 Baada ya muda mrefu,* mfalme wa Misri akafa,+ lakini Waisraeli wakaendelea kulia kwa uchungu kwa sababu ya utumwa na kupaza kilio cha malalamishi, na kilio chao cha kuomba msaada kwa sababu ya utumwa kikaendelea kupanda juu kwa Mungu wa kweli.+ 24 Mwishowe Mungu akasikia kilio chao cha uchungu,+ naye akakumbuka agano lake alilofanya na Abrahamu, Isaka, na Yakobo.+ 25 Basi Mungu akawakazia uangalifu Waisraeli; na Mungu akayaona mateso yao.
3 Musa akawa mchungaji wa kondoo wa Yethro,+ baba mkwe wake, kuhani wa Midiani. Alipokuwa akiwaongoza kondoo kuelekea upande wa magharibi wa nyika, hatimaye alifika kwenye mlima wa Mungu wa kweli ulioitwa Horebu.+ 2 Kisha malaika wa Yehova akamtokea katika mwali wa moto katikati ya kichaka cha miiba.+ Musa alipoendelea kutazama, aliona kwamba kichaka hicho cha miiba kilikuwa kikiwaka moto, lakini hakikuteketea. 3 Basi Musa akasema: “Nitaenda kuchunguza jambo hili la ajabu, nione kwa nini kichaka kile cha miiba hakiteketei.” 4 Yehova alipoona akienda kukitazama, Mungu akamwita kutoka katika kichaka cha miiba: “Musa! Musa!” naye akajibu: “Mimi hapa.” 5 Akamwambia: “Usikaribie zaidi. Vua viatu vyako, kwa sababu mahali unaposimama ni ardhi takatifu.”
6 Akaendelea kusema: “Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Abrahamu,+ Mungu wa Isaka,+ na Mungu wa Yakobo.”+ Ndipo Musa akauficha uso wake, kwa sababu aliogopa kumtazama Mungu wa kweli. 7 Kisha Yehova akasema: “Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walio Misri, nami nimesikia kilio chao kwa sababu ya wale wanaowalazimisha kufanya kazi; ninajua vema maumivu yao.+ 8 Nitashuka huko ili niwaokoe kutoka mikononi mwa Wamisri+ na kuwapandisha kutoka katika nchi hiyo na kuwapeleka katika nchi nzuri na kubwa, nchi inayotiririka maziwa na asali,+ eneo la Wakanaani, Wahiti, Waamori, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi.+ 9 Sasa tazama! Kilio cha Waisraeli kimenifikia, nami nimeona pia jinsi Wamisri wanavyowakandamiza kwa ukatili.+ 10 Sasa njoo, nitakutuma kwa Farao, nawe utawatoa watu wangu Waisraeli kutoka Misri.”+
11 Hata hivyo, Musa akamwambia Mungu wa kweli: “Mimi ni nani hata niende kwa Farao na kuwatoa Waisraeli nchini Misri?” 12 Mungu akamwambia: “Nitathibitika kuwa pamoja nawe,+ na hii ndiyo ishara itakayoonyesha kwamba ni mimi niliyekutuma: Baada ya kuwatoa Waisraeli nchini Misri, ninyi mtanitumikia* mimi, Mungu wa kweli, kwenye mlima huu.”+
13 Lakini Musa akamwambia Mungu wa kweli: “Tuseme niende kwa Waisraeli na kuwaambia, ‘Mungu wa mababu zenu amenituma kwenu,’ nao waniulize, ‘Jina lake ni nani?’+ Niwaambie nini?” 14 Basi Mungu akamwambia Musa: “Nitakuwa Kile Ninachochagua* Kuwa.”*+ Kisha akasema: “Hivi ndivyo unavyopaswa kuwaambia Waisraeli, ‘Nitakuwa amenituma kwenu.’”+ 15 Tena Mungu akamwambia Musa:
“Hivi ndivyo unavyopaswa kuwaambia Waisraeli, ‘Yehova Mungu wa mababu zenu, Mungu wa Abrahamu,+ Mungu wa Isaka,+ na Mungu wa Yakobo,+ amenituma kwenu.’ Hilo ndilo jina langu milele,+ na hivyo ndivyo ninavyopaswa kukumbukwa kizazi baada ya kizazi. 16 Sasa nenda, uwakusanye wazee wa Israeli na kuwaambia, ‘Yehova Mungu wa mababu zenu amenitokea, Mungu wa Abrahamu, Isaka, na Yakobo, naye alisema: “Hakika nimewatazama+ na nimeona mambo mnayotendewa nchini Misri. 17 Kwa hiyo ninasema, nitawatoa katika mateso+ mnayopata mikononi mwa Wamisri na kuwapeleka katika nchi ya Wakanaani, Wahiti, Waamori,+ Waperizi,+ Wahivi, na Wayebusi, nchi inayotiririka maziwa na asali.”’+
18 “Hakika wataisikiliza sauti yako,+ nawe utaenda, wewe pamoja na wazee wa Israeli, kwa mfalme wa Misri, nanyi mnapaswa kumwambia: ‘Yehova Mungu wa Waebrania+ amewasiliana nasi. Kwa hiyo, tafadhali, turuhusu tusafiri kwa siku tatu nyikani ili tumtolee Yehova Mungu wetu dhabihu.’+ 19 Lakini mimi mwenyewe ninajua vema kwamba mfalme wa Misri hatawaruhusu kwenda asipolazimishwa kwa mkono wenye nguvu.+ 20 Kwa hiyo nitalazimika kuunyoosha mkono wangu na kuipiga Misri kwa matendo yangu yote ya ajabu nitakayofanya nchini humo, kisha atawaruhusu mwondoke.+ 21 Nami nitawafanya watu hawa wapate kibali machoni pa Wamisri, nanyi mtakapoondoka, hamtaondoka kamwe mikono mitupu.+ 22 Kila mwanamke anapaswa kumwomba jirani yake na mwanamke anayeishi nyumbani mwake vito vya fedha na vya dhahabu na pia mavazi, nanyi mtawavika wana wenu na mabinti wenu; nanyi mtachukua mali za Wamisri.”+
4 Hata hivyo, Musa akamwambia: “Lakini tuseme kwamba hawaniamini wala kuisikiliza sauti yangu,+ kwa maana watasema, ‘Yehova hakukutokea.’” 2 Ndipo Yehova akamuuliza: “Ni nini hicho kilicho mkononi mwako?” Akajibu: “Fimbo.” 3 Akamwambia: “Itupe chini.” Basi akaitupa chini, nayo ikawa nyoka;+ Musa akamkimbia. 4 Ndipo Yehova akamwambia Musa: “Unyooshe mkono wako umkamate mkia.” Basi akaunyoosha mkono wake na kumkamata, nyoka huyo akawa fimbo mkononi mwake. 5 Kisha Mungu akamwambia: “Fanya hivyo ili waamini kwamba Yehova Mungu wa mababu zao, Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo,+ amekutokea.”+
6 Tena Yehova akamwambia: “Tafadhali, utie mkono wako ndani ya mkunjo wa juu wa vazi lako.” Basi akautia mkono wake ndani ya mkunjo wa vazi lake. Alipoutoa, tazama, mkono wake ulikuwa umepigwa na ukoma, ukawa mweupe kama theluji!+ 7 Kisha Mungu akamwambia: “Urudishe mkono wako kwenye mkunjo wa juu wa vazi lako.” Basi akaurudisha mkono wake ndani ya vazi lake. Alipoutoa katika vazi lake, ulikuwa umerudia hali yake na kuwa kama sehemu nyingine za mwili wake! 8 Mungu akasema: “Wasipokuamini au wakipuuza ishara ya kwanza, basi kwa hakika watatii ishara+ ya pili. 9 Lakini hata wasipoamini ishara hizo mbili na kukataa kuisikiliza sauti yako, utachota maji kutoka katika Mto Nile na kuyamwaga kwenye nchi kavu, na maji hayo yatakuwa damu kwenye nchi kavu.”+
10 Sasa Musa akamwambia Yehova: “Ee Yehova, niwie radhi, lakini sijawahi kuwa msemaji mwenye ufasaha, tangu zamani na hata baada ya wewe kuzungumza nami mtumishi wako, kwa maana mimi si msemaji mzuri* na ulimi wangu ni mzito.”+ 11 Yehova akamuuliza: “Ni nani aliyemuumbia mwanadamu kinywa, au ni nani anayewafanya wawe bubu, viziwi, waone vizuri, au wawe vipofu? Je, si mimi, Yehova? 12 Basi nenda sasa, nami nitakuwa pamoja nawe utakapokuwa ukizungumza,* nami nitakufundisha unalopaswa kusema.”+ 13 Lakini akasema: “Ee Yehova, niwie radhi, tafadhali, mtume yeyote unayetaka kumtuma.” 14 Ndipo hasira ya Yehova ikawaka dhidi ya Musa, akasema: “Namna gani ndugu yako Haruni,+ Mlawi? Ninajua kwamba anaweza kuzungumza vizuri sana. Na sasa yuko njiani anakuja hapa kukutana nawe. Atakapokuona, moyo wake utashangilia.+ 15 Basi unapaswa kuzungumza naye na kuweka maneno hayo kinywani mwake,+ nami nitakuwa pamoja nawe na yeye pia mnapozungumza,+ nami nitawafundisha jambo la kufanya. 16 Atazungumza na watu kwa niaba yako, naye atakuwa msemaji wako, nawe utakuwa kama Mungu kwake.*+ 17 Nawe utachukua fimbo hii mkononi mwako na kuitumia kufanya zile ishara.”+
18 Basi Musa akarudi kwa Yethro baba mkwe wake+ na kumwambia: “Ninataka kwenda, tafadhali, nirudi kwa ndugu zangu walio Misri nione kama wangali hai.” Yethro akamwambia Musa: “Nenda kwa amani.” 19 Basi Yehova akamwambia Musa huko Midiani: “Nenda, rudi Misri, kwa sababu watu wote waliotaka kukuua* wamekufa.”+
20 Kisha Musa akamchukua mke wake na wanawe na kuwapandisha juu ya punda, akaanza safari ya kurudi nchini Misri. Pia, Musa aliichukua ile fimbo ya Mungu wa kweli mkononi mwake. 21 Halafu Yehova akamwambia Musa: “Baada ya kurudi Misri, hakikisha kwamba unafanya mbele ya Farao miujiza yote ambayo nimekupa nguvu za kuifanya.+ Lakini nitauacha moyo wake uwe mkaidi,+ naye hatawaruhusu watu hao waondoke.+ 22 Unapaswa kumwambia Farao, ‘Hivi ndivyo Yehova anavyosema: “Israeli ni mwanangu, mzaliwa wangu wa kwanza.+ 23 Ninakwambia, Mruhusu mwanangu aondoke ili anitumikie. Lakini ukikataa kumruhusu aondoke, nitamuua mwana wako, mzaliwa wako wa kwanza.”’”+
24 Sasa walipokuwa njiani, mahali pa kulala, Yehova+ akakutana naye, na alikuwa akitafuta kumuua.+ 25 Hatimaye Sipora+ akachukua jiwe gumu lenye makali* na kumtahiri mwanawe, kisha akagusa miguu yake* kwa govi hilo na kusema: “Ni kwa sababu wewe ni bwana harusi wa damu kwangu.” 26 Basi Mungu akamwacha aende. Wakati huo Sipora akasema, “bwana harusi wa damu,” kwa sababu ya tohara hiyo.
27 Kisha Yehova akamwambia Haruni: “Nenda nyikani ukakutane na Musa.”+ Basi akaenda na kukutana naye kwenye mlima wa Mungu wa kweli+ na kumsalimu kwa busu. 28 Na Musa akamwambia Haruni maneno yote ya Yehova, aliyekuwa amemtuma,+ na ishara zote alizomwamuru afanye.+ 29 Kisha Musa na Haruni wakaenda kuwakusanya wazee wote wa Waisraeli.+ 30 Haruni akawaambia maneno yote ambayo Yehova alimwambia Musa, naye akafanya zile ishara+ machoni pa watu. 31 Kwa hiyo watu wakaamini.+ Waliposikia kwamba Yehova alikuwa amewaelekezea uangalifu Waisraeli+ na kwamba alikuwa ameona mateso yao,+ wakainama chini na kusujudu.
5 Baadaye, Musa na Haruni wakaenda kwa Farao na kumwambia: “Hivi ndivyo anavyosema Yehova Mungu wa Israeli, ‘Waruhusu watu wangu waende ili wanifanyie sherehe nyikani.’” 2 Lakini Farao akasema: “Yehova ni nani,+ hivi kwamba nitii sauti yake na kuwaruhusu Waisraeli waende zao?+ Simjui Yehova kamwe, na isitoshe, sitawaruhusu Waisraeli waende zao.”+ 3 Lakini wakamwambia: “Mungu wa Waebrania amewasiliana nasi. Tafadhali, tungependa kusafiri kwa siku tatu kwenda nyikani tukamtolee dhabihu Yehova Mungu wetu;+ tusipofanya hivyo, atatupiga kwa ugonjwa au kwa upanga.” 4 Mfalme wa Misri akawaambia: “Musa na Haruni, kwa nini mnawafanya watu waache kazi zao? Rudini mkafanye kazi yenu!”*+ 5 Farao akaendelea kusema: “Angalieni jinsi watu walivyo wengi nchini, nanyi mnataka kuwafanya waache kazi yao.”
6 Siku hiyohiyo, Farao akawaamuru hivi wasimamizi wa kazi na wasimamizi wa watumwa: 7 “Msiwape tena watu hawa nyasi za kufyatua matofali.+ Waacheni wakajitafutie nyasi wenyewe. 8 Lakini bado mnapaswa kuwaamuru wafyatue idadi ileile ya matofali kama awali. Msiwapunguzie idadi, kwa sababu wanastarehe.* Ndiyo sababu wanalia, ‘Tunataka kwenda, tunataka kumtolea dhabihu Mungu wetu!’ 9 Watumikisheni zaidi, wapeni kazi zaidi ili wasisikilize uwongo.”
10 Basi wasimamizi wa kazi+ na wasimamizi wa watumwa wakaenda na kuwaambia watu: “Hivi ndivyo Farao anavyosema, ‘Siwapi tena nyasi. 11 Nendeni mkajitafutie nyasi zenu wenyewe popote mtakapozipata, lakini kazi yenu haitapunguzwa hata kidogo.’” 12 Ndipo watu wakatawanyika kotekote katika nchi ya Misri ili kukusanya vishina vya mabua ili waweze kupata nyasi. 13 Na wasimamizi wa kazi waliendelea kusisitiza hivi: “Ni lazima kila mmoja wenu amalize kazi yake kila siku, kama mlivyokuwa mkifanya mlipokuwa mkiletewa nyasi.” 14 Pia, wasimamizi wa Waisraeli, ambao walikuwa wamechaguliwa na wasimamizi wa kazi waliowekwa na Farao kuwasimamia wasimamizi hao wa Waisraeli, walipigwa.+ Waliwauliza: “Kwa nini hamkufyatua idadi ileile ya matofali mliyokuwa mkifyatua mwanzoni? Hamkufanya hivyo jana na leo.”
15 Ndipo wasimamizi wa Waisraeli wakaenda kumlalamikia Farao, wakisema: “Kwa nini unatutendea hivi sisi watumishi wako? 16 Sisi watumishi wako hatupewi nyasi zozote, lakini wanatuambia, ‘Fyatueni matofali!’ Tunapigwa, lakini kosa ni la watu wako.” 17 Lakini Farao akawaambia: “Mnastarehe,* mnastarehe!*+ Ndiyo sababu mnasema, ‘Tunataka kwenda, tunataka kumtolea Yehova dhabihu.’+ 18 Basi sasa, rudini kazini! Hamtapewa nyasi zozote, lakini ni lazima mfyatue idadi ileile ya matofali.”
19 Kwa hiyo wasimamizi wa Waisraeli wakatambua kwamba wako katika shida kubwa kwa sababu ya amri hii: “Msipunguze hata kidogo idadi ya matofali mnayopaswa kufyatua kila siku.” 20 Walipotoka kwa Farao walikutana na Musa na Haruni, waliokuwa wamesimama wakiwangojea. 21 Mara moja wasimamizi hao wakawaambia: “Yehova na awatazame ninyi na kuwahukumu, kwa maana mmefanya Farao na watumishi wake watudharau* nanyi mmeweka upanga mkononi mwao ili watuue.”+ 22 Kisha Musa akamgeukia Yehova na kumuuliza: “Yehova, kwa nini umewatesa watu hawa? Kwa nini umenituma? 23 Tangu nilipofika mbele ya Farao kuzungumza katika jina lako,+ amewatesa vikali zaidi watu hawa,+ nawe hakika hujawaokoa watu wako.”+
6 Basi Yehova akamwambia Musa: “Sasa utaona mambo nitakayomtendea Farao.+ Mkono wenye nguvu utamlazimisha awaruhusu watu wangu waende zao, na mkono wenye nguvu utamlazimisha awafukuze kutoka katika nchi yake.”+
2 Kisha Mungu akamwambia Musa: “Mimi ni Yehova. 3 Nami nilikuwa nikimtokea Abrahamu, Isaka, na Yakobo kama Mungu Mweza-Yote,+ lakini kwa jina langu Yehova+ sikujitambulisha kwao.+ 4 Pia, nilifanya agano pamoja nao kwamba nitawapa nchi ya Kanaani, nchi ambamo waliishi kama wageni.+ 5 Sasa mimi mwenyewe nimesikia kilio cha uchungu cha Waisraeli, ambao Wamisri wanawatumikisha kama watumwa, nami ninakumbuka agano langu.+
6 “Kwa hiyo, waambie Waisraeli: ‘Mimi ni Yehova, nami nitawatoa kutoka chini ya mizigo ya Wamisri na kuwaokoa kutoka katika utumwa wao,+ nami nitawakomboa kwa mkono ulionyooshwa* na kwa hukumu kubwa.+ 7 Nami nitawachukua muwe watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu,+ nanyi hakika mtajua kwamba mimi ni Yehova Mungu wenu anayewatoa kutoka chini ya mizigo ya Misri. 8 Nami nitawapeleka katika nchi niliyoapa* kwamba nitampa Abrahamu, Isaka, na Yakobo; nitawapa ninyi iwe miliki yenu.+ Mimi ni Yehova.’”+
9 Baadaye Musa akawapa Waisraeli ujumbe huo, lakini hawakumsikiliza Musa kwa sababu walikuwa wamevunjika moyo na kwa sababu ya utumwa wa kikatili.+
10 Kisha Yehova akamwambia Musa: 11 “Nenda ukamwambie Farao, mfalme wa Misri, kwamba anapaswa kuwaruhusu Waisraeli waondoke katika nchi yake.” 12 Lakini Musa akamwambia Yehova: “Tazama! Waisraeli hawajanisikiliza,+ Farao atanisikilizaje mimi, mtu asiye na ufasaha?”*+ 13 Lakini Yehova akawaambia tena Musa na Haruni amri wanazopaswa kuwapa Waisraeli na pia Farao, mfalme wa Misri, ili kuwatoa Waisraeli katika nchi ya Misri.
14 Hawa ndio viongozi wa nyumba ya baba zao: Wana wa Rubeni, mzaliwa wa kwanza wa Israeli,+ walikuwa Hanoki, Palu, Hezroni, na Karmi.+ Hizo ndizo koo za Rubeni.
15 Wana wa Simeoni walikuwa Yemueli, Yamini, Ohadi, Yakini, Zohari, na Shauli, mwana wa mwanamke Mkanaani.+ Hizo ndizo koo za Simeoni.
16 Haya ndiyo majina ya wana wa Lawi,+ kulingana na koo zao: Gershoni, Kohathi, na Merari.+ Lawi aliishi miaka 137.
17 Wana wa Gershoni walikuwa Libni na Shimei, kulingana na koo zao.+
18 Wana wa Kohathi walikuwa Amramu, Ishari, Hebroni, na Uzieli.+ Kohathi aliishi miaka 133.
19 Wana wa Merari walikuwa Mali na Mushi.
Hizo ndizo zilizokuwa koo za Walawi, kulingana na nasaba ya koo zao.+
20 Sasa Amramu alimwoa Yokebedi, dada ya baba yake.+ Akamzalia Amramu wana hawa: Haruni na Musa.+ Amramu aliishi miaka 137.
21 Wana wa Ishari walikuwa Kora,+ Nefegi, na Zikri.
22 Wana wa Uzieli walikuwa Mishaeli, Elsafani,+ na Sithri.
23 Sasa Haruni alimwoa Elisheba, binti ya Aminadabu, dada ya Nashoni.+ Akamzalia Haruni wana hawa: Nadabu, Abihu, Eleazari, na Ithamari.+
24 Wana wa Kora walikuwa Asiri, Elkana, na Abiasafu.+ Hizo ndizo zilizokuwa koo za Wakora.+
25 Eleazari,+ mwana wa Haruni, alimwoa mmoja wa mabinti wa Putieli. Akamzalia mwana aliyeitwa Finehasi.+
Hao ndio viongozi wa koo* za Walawi, kulingana na koo zao.+
26 Hao ndio Haruni na Musa walioambiwa na Yehova: “Watoeni Waisraeli katika nchi ya Misri, kundi kwa kundi.”*+ 27 Hao ndio waliozungumza na Farao, mfalme wa Misri, ili awaruhusu Waisraeli watoke Misri. Ilikuwa huyu Musa na Haruni.+
28 Siku hiyo ambayo Yehova alizungumza na Musa katika nchi ya Misri, 29 Yehova alimwambia Musa: “Mimi ni Yehova. Mwambie Farao, mfalme wa Misri, kila jambo ninalokwambia.” 30 Kisha Musa akamwambia Yehova: “Tazama! sina ufasaha,* sasa Farao atanisikilizaje?”+
7 Kisha Yehova akamwambia Musa: “Tazama, nimekufanya kuwa kama Mungu* kwa Farao, na Haruni ndugu yako atakuwa nabii wako.+ 2 Unapaswa kurudia kila jambo nitakalokuamuru, na Haruni ndugu yako atazungumza na Farao, naye Farao atawaruhusu Waisraeli watoke katika nchi yake. 3 Lakini mimi, nitauacha moyo wa Farao uwe mkaidi,+ nami nitazidisha ishara zangu na miujiza yangu katika nchi ya Misri.+ 4 Lakini Farao hatawasikiliza ninyi, nami nitauweka mkono wangu juu ya Misri na kuyatoa makundi yangu makubwa,* watu wangu, Waisraeli, kutoka katika nchi ya Misri kwa hukumu kubwa.+ 5 Na Wamisri watajua kwa hakika kwamba mimi ni Yehova+ nitakapounyoosha mkono wangu dhidi ya Misri na kuwatoa Waisraeli miongoni mwao.” 6 Musa na Haruni wakafanya mambo ambayo Yehova aliwaamuru; hivyo ndivyo walivyofanya. 7 Musa alikuwa na umri wa miaka 80 naye Haruni alikuwa na umri wa miaka 83 walipozungumza na Farao.+
8 Sasa Yehova akamwambia Musa na Haruni: 9 “Farao akiwaambia, ‘Fanyeni muujiza,’ mwambie Haruni, ‘Chukua fimbo yako uitupe chini mbele ya Farao.’ Itakuwa nyoka mkubwa.”+ 10 Basi Musa na Haruni wakaenda kwa Farao na kufanya kama tu Yehova alivyokuwa amewaamuru. Haruni akaitupa chini fimbo yake mbele ya Farao na watumishi wake, nayo ikawa nyoka mkubwa. 11 Hata hivyo, Farao akawaita watu wenye hekima na walozi, na makuhani wachawi wa Misri+ nao pia wakafanya muujiza huohuo kwa uchawi wao.*+ 12 Kila mmoja wao akatupa chini fimbo yake, nazo zikawa nyoka wakubwa; lakini fimbo ya Haruni ikazimeza fimbo zao. 13 Lakini moyo wa Farao uliendelea kuwa mkaidi,+ na kama Yehova alivyosema, Farao hakuwasikiliza.
14 Ndipo Yehova akamwambia Musa: “Moyo wa Farao ni mgumu.+ Amekataa kuwaruhusu watu wangu waende zao. 15 Nenda kwa Farao asubuhi. Tazama! Anaenda mtoni! Unapaswa kusimama kwenye ukingo wa Mto Nile; na ubebe mkononi ile fimbo iliyogeuka kuwa nyoka.+ 16 Nawe unapaswa kumwambia, ‘Yehova Mungu wa Waebrania amenituma kwako,+ naye anasema: “Waruhusu watu wangu waende ili wanitumikie nyikani,” lakini mpaka sasa hujatii. 17 Yehova anasema hivi: “Kwa jambo hili utajua kwamba mimi ni Yehova.+ Tazama ninayapiga maji ya Mto Nile kwa fimbo hii iliyo mkononi mwangu, nayo yatabadilika na kuwa damu. 18 Samaki walio katika Mto Nile watakufa, nao Mto Nile utanuka, na Wamisri watashindwa kunywa maji ya Mto Nile.”’”
19 Kisha Yehova akamwambia Musa: “Mwambie Haruni, ‘Ichukue fimbo yako na uunyooshe mkono wako juu ya maji yote ya Misri,+ juu ya mito yake, juu ya mifereji yake,* juu ya maeneo yake yenye umajimaji,+ na juu ya mabwawa yake yote, ili yawe damu.’ Kutakuwa na damu katika nchi yote ya Misri, hata katika vyombo vya mbao na vya mawe.” 20 Mara moja Musa na Haruni wakafanya kama Yehova alivyowaamuru. Akaiinua fimbo hiyo na kuyapiga maji ya Mto Nile mbele ya Farao na watumishi wake, na maji yote yaliyokuwa katika Mto Nile yakabadilika na kuwa damu.+ 21 Basi samaki waliokuwa mtoni wakafa,+ na mto ukaanza kunuka, na Wamisri hawakuweza kunywa maji ya Mto Nile,+ kulikuwa na damu katika nchi yote ya Misri.
22 Lakini makuhani wachawi wa Misri wakafanya jambo hilohilo kwa mazingaombwe yao,+ hivi kwamba moyo wa Farao ukaendelea kuwa mkaidi, na kama Yehova alivyosema, Farao hakuwasikiliza.+ 23 Basi Farao akarudi nyumbani kwake, wala hakuzingatia jambo hilo moyoni mwake. 24 Kwa hiyo, Wamisri wote walikuwa wakichimba kandokando kuzunguka Mto Nile wakitafuta maji ya kunywa, kwa sababu hawangeweza kunywa maji yoyote ya Mto Nile. 25 Na siku saba kamili zikapita baada ya Yehova kuupiga Mto Nile.
8 Kisha Yehova akamwambia Musa: “Nenda kwa Farao umwambie, ‘Yehova anasema hivi: “Waruhusu watu wangu waende wakanitumikie.+ 2 Ukiendelea kukataa kuwaruhusu waondoke, nitaleta pigo la vyura katika eneo lako lote.+ 3 Nao Mto Nile utajaa vyura, nao watatoka humo na kuingia ndani ya nyumba yako, ndani ya chumba chako cha kulala, kitandani mwako, katika nyumba za watumishi wako na juu ya watu wako, ndani ya majiko yenu, na ndani ya vyombo vyenu vya* kukandia unga.+ 4 Vyura watapanda juu yako, juu ya watu wako, na juu ya watumishi wako wote.”’”
5 Baadaye Yehova akamwambia Musa: “Mwambie Haruni, ‘Unyooshe mkono wako ulio na fimbo juu ya mito, mifereji ya Nile, na maeneo yenye umajimaji, ili vyura waje juu ya nchi ya Misri.’” 6 Basi Haruni akaunyoosha mkono wake juu ya maji ya Misri, na vyura wakaanza kuja na kuifunika nchi ya Misri. 7 Hata hivyo, makuhani wachawi wakafanya jambo hilohilo kwa mazingaombwe yao, nao pia wakafanya vyura waje juu ya nchi ya Misri.+ 8 Ndipo Farao akawaita Musa na Haruni na kuwaambia: “Msihini Yehova aniondolee mimi na watu wangu vyura hawa,+ kwa maana ninataka kuwaruhusu watu waende zao wakamtolee Yehova dhabihu.” 9 Kisha Musa akamwambia Farao: “Kwa heshima yako niambie wakati unaotaka nimwombe Mungu awaondoe vyura kutoka kwako, kutoka kwa watumishi wako, kutoka kwa watu wako, na kutoka katika nyumba zenu. Watabaki katika Mto Nile tu.” 10 Farao akamwambia: “Kesho.” Basi Musa akasema: “Itakuwa kama unavyosema, ili ujue kwamba hakuna yeyote aliye kama Yehova Mungu wetu.+ 11 Vyura wataondoka kwako, katika nyumba zako, kutoka kwa watumishi wako, na kutoka kwa watu wako. Watabaki katika Mto Nile tu.”+
12 Basi Musa na Haruni wakaondoka mbele ya Farao, naye Musa akamsihi Yehova amwondolee Farao vyura aliomletea.+ 13 Kisha Yehova akafanya kama Musa alivyomwomba, na vyura wakaanza kufia nyumbani, nyuani, na mashambani. 14 Watu wakakusanya marundo yasiyohesabika ya vyura, na nchi ikaanza kunuka. 15 Farao alipoona kwamba hali ni nafuu, akaufanya moyo wake kuwa mgumu,+ na kama Yehova alivyosema, Farao akakataa kuwasikiliza.
16 Sasa Yehova akamwambia Musa: “Mwambie Haruni, ‘Inyooshe fimbo yako na uyapige mavumbi ya ardhi, nayo yatakuwa mbu* katika nchi yote ya Misri.’” 17 Nao wakafanya hivyo. Haruni akaunyoosha mkono wake uliokuwa na fimbo yake na kuyapiga mavumbi ya ardhi, na mbu wakawavamia wanadamu na wanyama. Mavumbi yote katika nchi yote ya Misri yakawa mbu.+ 18 Makuhani wachawi wakajaribu pia kugeuza mavumbi yawe mbu kwa mazingaombwe yao,+ lakini hawakuweza. Mbu hao wakawavamia wanadamu na wanyama. 19 Basi makuhani wachawi wakamwambia Farao: “Ni kidole cha Mungu!”+ Lakini moyo wa Farao ukaendelea kuwa mkaidi, na kama Yehova alivyosema, hakuwasikiliza.
20 Kisha Yehova akamwambia Musa: “Amka asubuhi na mapema ukasimame mbele ya Farao. Tazama! Anaenda mtoni! Nawe unapaswa kumwambia, ‘Yehova anasema hivi: “Waruhusu watu wangu waende wakanitumikie. 21 Lakini usipowaruhusu watu wangu waende zao, nitakuletea nzi,* wewe, watumishi wako, na watu wako, nao wataingia katika nyumba zako; na nyumba za Misri zitajaa nzi hao, nao wataifunika hata ardhi ambayo Wamisri wamesimama juu yake. 22 Siku hiyo, hakika nitaitenga nchi ya Gosheni, wanakoishi watu wangu. Hakuna nzi yeyote atakayepatikana huko,+ na kwa jambo hilo utajua kwamba mimi, Yehova, niko humu nchini.+ 23 Nami nitatofautisha kati ya watu wangu na watu wako. Kesho ishara hii itatokea.”’”
24 Basi Yehova akafanya kama alivyosema, na makundi makubwa sana ya nzi yakaanza kuvamia nyumba ya Farao na nyumba za watumishi wake na nchi yote ya Misri.+ Nchi ikaharibiwa na nzi hao.+ 25 Hatimaye Farao akawaita Musa na Haruni na kuwaambia: “Nendeni, mkamtolee dhabihu Mungu wenu nchini.” 26 Lakini Musa akasema: “Si vema kufanya hivyo, kwa sababu dhabihu tutakazomtolea Yehova Mungu wetu zitawachukiza Wamisri.+ Tukitoa dhabihu zinazowachukiza Wamisri mbele ya macho yao, je, hawatatupiga mawe? 27 Tutasafiri kwa siku tatu nyikani, na huko tutamtolea Yehova Mungu wetu dhabihu kama alivyotuambia.”+
28 Basi Farao akasema: “Nitawaruhusu mwende mkamtolee Yehova Mungu wenu dhabihu nyikani. Ila tu, msiende mbali sana. Msihini Mungu kwa niaba yangu.”+ 29 Musa akasema: “Sasa ninaenda zangu, nami nitamsihi Yehova, na kesho nzi wataondoka kwako Farao, kwa watumishi wako, na kwa watu wako. Lakini wewe, Ee Farao, unapaswa kuacha kutuchezea* kwa kukataa kuturuhusu kwenda kumtolea Yehova dhabihu.”+ 30 Kisha Musa akaondoka mbele ya Farao na kumsihi Yehova.+ 31 Basi Yehova akafanya kama Musa alivyomsihi, na nzi wakaondoka kwa Farao, kwa watumishi wake, na kwa watu wake. Hakubaki hata nzi mmoja. 32 Hata hivyo, kwa mara nyingine tena Farao akaufanya moyo wake kuwa mgumu naye hakuwaruhusu Waisraeli waende zao.
9 Kwa hiyo Yehova akamwambia Musa: “Nenda kwa Farao umwambie, ‘Yehova Mungu wa Waebrania anasema hivi: “Waruhusu watu wangu waende wakanitumikie.+ 2 Lakini ukikataa kuwaruhusu waende zao, na ukiendelea kuwazuia, 3 tazama! mkono wangu mimi Yehova+ utaipiga mifugo yenu iliyo shambani. Nitawaletea pigo kali sana farasi, punda, ngamia, ng’ombe, na makundi yenu.+ 4 Na hakika mimi Yehova nitaitofautisha mifugo ya Waisraeli na mifugo ya Wamisri, na hakuna mnyama yeyote wa Waisraeli atakayekufa.”’”+ 5 Zaidi ya hayo, Yehova aliweka wakati hususa, akasema: “Kesho, mimi Yehova nitafanya jambo hilo katika nchi hii.”
6 Na kesho yake Yehova akafanya hivyo, kila aina ya mifugo ya Wamisri ikaanza kufa,+ lakini hakuna mnyama hata mmoja wa Waisraeli aliyekufa. 7 Farao alipouliza, aliambiwa kwamba hakuna mnyama hata mmoja wa Waisraeli aliyekufa. Hata hivyo, moyo wa Farao ukaendelea kuwa mgumu, naye hakuwaruhusu Waisraeli waende zao.+
8 Kisha Yehova akawaambia Musa na Haruni: “Jazeni masizi ya tanuru* kwenye mikono yenu miwili, Musa anapaswa kuyarusha hewani mbele ya Farao. 9 Nayo yatakuwa mavumbi laini juu ya nchi yote ya Misri, kisha yatakuwa majipu yenye usaha kwenye miili ya wanadamu na wanyama katika nchi yote ya Misri.”
10 Basi wakachukua masizi kutoka katika tanuru* na kusimama mbele ya Farao, naye Musa akayarusha hewani, nayo yakawa majipu yenye usaha yaliyotokea kwenye miili ya wanadamu na wanyama. 11 Makuhani wachawi hawakuweza kusimama mbele ya Musa kwa sababu ya majipu hayo, kwa maana makuhani wachawi na Wamisri wote walikuwa wamepatwa na majipu hayo.+ 12 Lakini Yehova akauacha moyo wa Farao uwe mkaidi, na kama Yehova alivyokuwa amemwambia Musa, Farao hakuwasikiliza.+
13 Kisha Yehova akamwambia Musa: “Amka asubuhi na mapema uende ukasimame mbele ya Farao, umwambie, ‘Yehova Mungu wa Waebrania amesema hivi: “Waruhusu watu wangu waende wakanitumikie. 14 Kwa maana sasa ninayaelekeza mapigo yangu yote niupige moyo wako, niwapige watumishi wako, na watu wako, ili ujue kwamba hakuna yeyote aliye kama mimi katika dunia yote.+ 15 Kwa maana kufikia sasa ningekuwa nimeunyoosha mkono wangu kwa nguvu na kukupiga wewe na watu wako kwa pigo kali sana, nawe ungekuwa umefutiliwa* mbali kutoka duniani. 16 Lakini nimekuacha uendelee kuishi kwa sababu hii hasa: ili nikuonyeshe nguvu zangu na ili jina langu litangazwe katika dunia yote.+ 17 Je, bado unatenda kwa kiburi dhidi ya watu wangu kwa kukataa kuwaruhusu waende zao? 18 Tazama, kesho wakati kama huu, nitaleta mvua kubwa sana ya mawe ambayo haijawahi kuonekana katika nchi ya Misri tangu mwanzo wake mpaka sasa. 19 Kwa hiyo, waambie watu watoe mifugo yote na vitu vyenu vyote vilivyo shambani na kuviingiza ndani ya nyumba. Kila mwanadamu na mnyama ambaye atapatikana shambani na ambaye hatakuwa ameingizwa ndani ya nyumba atakufa mvua hiyo ya mawe itakapomnyeshea.”’”
20 Mtumishi yeyote wa Farao aliyeogopa neno la Yehova aliwaingiza haraka watumishi wake na mifugo yake ndani ya nyumba, 21 lakini yeyote ambaye hakuzingatia moyoni mwake neno la Yehova aliwaacha watumishi wake na mifugo yake shambani.
22 Sasa Yehova akamwambia Musa: “Unyooshe mkono wako kuelekea mbinguni, ili mvua ya mawe inyeshe juu ya nchi yote ya Misri,+ iwanyeshee wanadamu na wanyama na mimea yote ya shambani nchini Misri.”+ 23 Kwa hiyo Musa akainyoosha fimbo yake kuelekea mbinguni, na Yehova akaleta ngurumo na mvua ya mawe, na moto* ukashuka duniani, na Yehova akafanya mvua ya mawe iendelee kunyesha juu ya nchi ya Misri. 24 Kulikuwa na mvua ya mawe, na moto ulikuwa ukiwakawaka katikati ya mvua hiyo. Mvua hiyo ilikuwa kubwa sana; mvua kama hiyo haikuwa imewahi kuonekana Misri tangu nchi hiyo iwe taifa.+ 25 Mvua hiyo ya mawe ilipiga kila kitu kilichokuwa shambani katika nchi yote ya Misri, kuanzia mwanadamu mpaka mnyama, iliharibu kabisa mimea yote na kuvunjavunja miti yote ya shambani.+ 26 Ila tu mvua hiyo ya mawe haikunyesha katika nchi ya Gosheni, ambako Waisraeli waliishi.+
27 Basi Farao akaamuru Musa na Haruni waitwe, akawaambia: “Wakati huu nimetenda dhambi. Yehova ni mwadilifu, lakini mimi na watu wangu tumekosea. 28 Msihini Yehova ili radi na mvua hii ya mawe kutoka kwa Mungu ikome. Kisha nitakuwa tayari kuwaruhusu mwende zenu, hamtakaa tena zaidi.” 29 Kwa hiyo Musa akamwambia: “Mara tu nitakapoondoka jijini, nitainyoosha mikono yangu mbele za Yehova. Ngurumo itakoma na mvua ya mawe haitaendelea kunyesha, ili ujue kwamba dunia ni ya Yehova.+ 30 Lakini tayari ninajua kwamba hata nikifanya hivyo, wewe na watumishi wako hamtamwogopa Yehova Mungu.”
31 Sasa mimea ya kitani na shayiri ilikuwa imeharibiwa kabisa na mvua, kwa sababu mimea ya shayiri ilikuwa na masuke na mimea ya kitani ilikuwa imechanua maua. 32 Lakini ngano na kusemethi* haikuwa imeharibiwa, kwa sababu haikuwa imekomaa.* 33 Basi Musa akaondoka jijini kutoka mbele ya Farao, akainyoosha mikono yake mbele za Yehova, ngurumo na mvua ya mawe zikakoma na mvua ikaacha kunyesha nchini.+ 34 Farao alipoona kwamba mvua ya mawe, na ngurumo zimekoma, akatenda dhambi tena na kuufanya moyo wake uwe mgumu,+ yeye pamoja na watumishi wake. 35 Na moyo wa Farao ukaendelea kuwa mkaidi, na kama Yehova alivyokuwa amesema kupitia Musa, Farao hakuwaruhusu Waisraeli waende zao.+
10 Kisha Yehova akamwambia Musa: “Nenda kwa Farao, kwa sababu nimeacha moyo wake na mioyo ya watumishi wake iwe migumu,+ ili nifanye ishara hizi zangu mbele yake,+ 2 na ili uwatangazie wanao na wajukuu wako jinsi nilivyoiadhibu vikali Misri na ishara nilizofanya miongoni mwenu;+ nanyi hakika mtajua kwamba mimi ni Yehova.”
3 Basi Musa na Haruni wakaenda kwa Farao na kumwambia: “Yehova Mungu wa Waebrania amesema hivi: ‘Utakataa mpaka lini kujinyenyekeza kwangu?+ Waruhusu watu wangu waende wakanitumikie. 4 Kwa maana ukiendelea kukataa kuwaruhusu watu wangu waende zao, kesho nitaleta nzige ndani ya mipaka yenu. 5 Nao wataifunika ardhi yote, hivi kwamba hamtaweza kuiona ardhi. Watakula kabisa mimea ambayo haikuharibiwa na mvua ya mawe ambayo mlibaki nayo, nao watakula miti yenu yote inayomea shambani.+ 6 Watajaa ndani ya nyumba zako, nyumba za watumishi wako wote, na nyumba zote za Misri, kwa kadiri ambayo baba zenu na mababu zenu hawajawahi kamwe kuona tangu walipozaliwa katika nchi hii mpaka leo.’”+ Kisha akageuka na kuondoka mbele ya Farao.
7 Ndipo watumishi wa Farao wakamwambia: “Mtu huyu ataendelea kututesa* mpaka lini? Waruhusu watu hawa waende zao wakamtumikie Yehova Mungu wao. Je, bado huoni kwamba Misri imeharibiwa?” 8 Kwa hiyo Musa na Haruni wakarudishwa kwa Farao, akawaambia: “Nendeni, mkamtumikie Yehova Mungu wenu. Lakini ni nani hasa watakaoenda?” 9 Musa akamjibu: “Tutaenda na vijana wetu, wazee wetu, wana wetu, mabinti wetu, kondoo wetu, na ng’ombe wetu,+ kwa maana tutamfanyia Yehova sherehe.”+ 10 Akawaambia: “Ikiwa nitawaruhusu ninyi na watoto wenu mwende, basi kwa kweli Yehova yuko pamoja nanyi!+ Ni wazi kwamba mnakusudia kutenda jambo fulani ovu. 11 Hapana! Ni wanaume wenu peke yao watakaoenda kumtumikia Yehova, kwa sababu hilo ndilo mliloomba.” Basi wakafukuzwa kutoka mbele ya Farao.
12 Sasa Yehova akamwambia Musa: “Unyooshe mkono wako juu ya nchi ya Misri ili nzige waje juu ya nchi ya Misri na kula mimea yote nchini, kila kitu ambacho hakikuharibiwa na mvua ya mawe.” 13 Mara moja Musa akainyoosha fimbo yake juu ya nchi ya Misri, na Yehova akasababisha upepo wa mashariki uvume nchini mchana kutwa na usiku kucha. Asubuhi ilipofika, upepo huo wa mashariki ukaleta nzige. 14 Na nzige hao wakaja juu ya nchi yote ya Misri na kufunika eneo lote la Misri.+ Walikuwa wengi kupindukia;+ nzige wengi sana hivyo hawakuwa wamewahi kuonekana, wala nzige wengi sana hivyo hawangeonekana tena kamwe. 15 Waliifunika nchi yote, na nchi ikawa na giza kwa sababu yao; walitafuna mimea yote nchini na matunda yote mitini ambayo hayakuharibiwa na mvua ya mawe; hakuna majani yoyote yaliyobaki mitini wala kwenye mimea ya shambani katika nchi yote ya Misri.
16 Basi Farao akawaita haraka Musa na Haruni na kuwaambia: “Nimemtendea dhambi Yehova Mungu wenu na ninyi pia. 17 Sasa, tafadhali, mnisamehe dhambi yangu mara hii moja tu, na kumsihi Yehova Mungu wenu angalau aniondolee pigo hili hatari.” 18 Basi akaondoka* kwa Farao na kumsihi Yehova.+ 19 Kisha Yehova akasababisha upepo huo ubadili mkondo, nao ukawa upepo wenye nguvu sana wa magharibi, ukawapeperusha nzige hao na kuwapeleka katika Bahari Nyekundu. Hakuna nzige hata mmoja aliyebaki katika eneo lote la Misri. 20 Hata hivyo, Yehova aliuacha moyo wa Farao uwe mkaidi,+ naye hakuwaruhusu Waisraeli waende zao.
21 Basi Yehova akamwambia Musa: “Unyooshe mkono wako kuelekea mbinguni ili giza liifunike nchi ya Misri, giza zito sana hivi kwamba linaweza kuguswa.” 22 Mara moja Musa akaunyoosha mkono wake kuelekea mbinguni, na giza zito sana likaifunika nchi yote ya Misri kwa siku tatu.+ 23 Hawakuonana, na kwa siku tatu hakuna yeyote kati yao aliyeondoka mahali alipokuwa; lakini Waisraeli wote walikuwa na mwangaza katika makao yao.+ 24 Kisha Farao akamwita Musa na kumwambia: “Nendeni, mkamtumikie Yehova.+ Ni kondoo wenu na ng’ombe wenu tu watakaobaki. Hata watoto wenu wanaweza kwenda nanyi.” 25 Lakini Musa akasema: “Wewe mwenyewe tupatie dhabihu na matoleo ya kuteketezwa, nasi tutazitoa kwa Yehova Mungu wetu.+ 26 Tutaenda pia na mifugo yetu. Hatutamwacha mnyama yeyote,* kwa sababu tutawatoa dhabihu baadhi ya wanyama hao tunapomwabudu Yehova Mungu wetu, na hatujui ni mnyama gani tutakayemtolea Yehova kuwa dhabihu mpaka tutakapofika huko.” 27 Kwa hiyo Yehova akauacha moyo wa Farao uwe mkaidi, naye hakukubali kuwaruhusu waende zao.+ 28 Farao akamwambia: “Ondoka mbele yangu! Usithubutu kuuona uso wangu tena, kwa maana siku utakapouona uso wangu, utakufa.” 29 Ndipo Musa akasema: “Na iwe kama ulivyosema, sitathubutu kuuona uso wako tena.”
11 Ndipo Yehova akamwambia Musa: “Nitamletea Farao na Misri pigo moja zaidi. Baada ya pigo hilo atawaruhusu mwondoke hapa.+ Atakapowaruhusu mwondoke, atawafukuza kabisa kutoka hapa.+ 2 Sasa waambie watu kwamba wanaume wote na wanawake wote wanapaswa kuwaomba majirani wao vito vya fedha na dhahabu.”+ 3 Basi Yehova akawafanya watu wapate kibali machoni pa Wamisri. Isitoshe, wakati huo Musa mwenyewe alikuwa mtu anayeheshimiwa sana na watumishi wa Farao na watu wengine nchini Misri.
4 Basi Musa akasema: “Yehova amesema hivi: ‘Karibu katikati ya usiku, nitapita katikati ya Misri,+ 5 na kila mzaliwa wa kwanza katika nchi ya Misri atakufa,+ kuanzia mzaliwa wa kwanza wa Farao anayeketi kwenye kiti chake cha ufalme mpaka mzaliwa wa kwanza wa kijakazi anayesaga nafaka kwa jiwe la kusagia, na kila mzaliwa wa kwanza wa mifugo.+ 6 Katika nchi yote ya Misri, kutakuwa na kilio kikubwa ambacho hakijawahi kamwe kuonekana na wala hakitaonekana tena kamwe.+ 7 Lakini hakuna hata mbwa atakayewabwekea* Waisraeli, iwe ni wanadamu au mifugo yao, ili mjue kwamba mimi Yehova ninaweza kutofautisha kati ya Wamisri na Waisraeli.’+ 8 Na watumishi wako wote hakika watakuja mbele zangu na kuniinamia, wakisema, ‘Nenda, wewe na watu wote wanaokufuata.’+ Na baada ya hapo, nitaondoka.” Ndipo akatoka mbele ya Farao kwa hasira kali.
9 Kisha Yehova akamwambia Musa: “Farao hatakusikiliza,+ ili miujiza yangu iongezeke katika nchi ya Misri.”+ 10 Musa na Haruni walifanya miujiza hiyo yote mbele ya Farao,+ lakini Yehova aliuacha moyo wa Farao uwe mkaidi, hivi kwamba hakuwaruhusu Waisraeli waondoke katika nchi yake.+
12 Sasa Yehova akawaambia Musa na Haruni katika nchi ya Misri: 2 “Mwezi huu utakuwa kwenu mwanzo wa miezi. Utakuwa mwezi wa kwanza wa mwaka kwenu.+ 3 Liambieni kusanyiko lote la Waisraeli hivi: ‘Siku ya kumi ya mwezi huu, kila mmoja wao anapaswa kuchukua kondoo kwa ajili ya nyumba ya baba yake, kondoo+ mmoja kwa kila nyumba. 4 Lakini ikiwa familia ina watu wachache hivi kwamba hawawezi kummaliza kondoo mmoja, watagawana* na jirani yao wa karibu ndani ya nyumba yao kulingana na idadi ya watu.* Mnapofanya hesabu, kadirieni kiasi cha nyama ya kondoo kitakacholiwa na kila mtu. 5 Kondoo wenu anapaswa kuwa kondoo dume wa mwaka mmoja, asiye na kasoro.+ Mnaweza kuchagua mwanakondoo dume au mwanambuzi. 6 Mtamtunza mpaka siku ya 14 ya mwezi huu,+ na familia zote katika kusanyiko la Israeli zinapaswa kumchinja jioni kabla ya giza kuingia.*+ 7 Watachukua kiasi fulani cha damu na kuinyunyiza kwenye miimo miwili ya mlango na kwenye kizingiti cha juu cha mlango wa nyumba ambamo watamla mnyama huyo.+
8 “‘Ni lazima waile nyama hiyo usiku huo.+ Wanapaswa kuichoma juu ya moto na kuila pamoja na mikate isiyo na chachu+ na mboga chungu za majani.+ 9 Msile sehemu yoyote ya nyama hiyo ikiwa mbichi au ikiwa imechemshwa, yaani, ikiwa imepikwa kwa maji, lakini ichomeni juu ya moto, kichwa chake pamoja na miguu yake na viungo vyake vya ndani. 10 Hampaswi kuhifadhi sehemu yoyote ya nyama hiyo mpaka asubuhi, lakini sehemu yoyote itakayobaki mpaka asubuhi mnapaswa kuiteketeza kwa moto.+ 11 Na hivi ndivyo mnavyopaswa kuila, mkiwa mmejifunga mishipi,* mkiwa na viatu miguuni, na mkiwa na fimbo zenu mkononi; nanyi mnapaswa kuila haraka. Ni Pasaka ya Yehova. 12 Kwa maana nitapita katikati ya nchi ya Misri usiku huo na kumuua kila mzaliwa wa kwanza katika nchi ya Misri, kuanzia mwanadamu mpaka mnyama;+ nami nitatekeleza hukumu dhidi ya miungu yote ya Misri.+ Mimi ni Yehova. 13 Ile damu itakuwa ishara inayoonyesha nyumba mtakazokuwamo; nami nitaiona damu hiyo na kupita juu yenu, na pigo halitawajia na kuwaangamiza ninyi nitakapoipiga nchi ya Misri.+
14 “‘Siku hiyo itakuwa ukumbusho kwenu, nanyi mnapaswa kuisherehekea ikiwa sherehe kwa Yehova katika vizazi vyenu vyote. Kwa kuwa ni sheria ya kudumu, mnapaswa kuisherehekea. 15 Kwa siku saba mtakula mikate isiyo na chachu.+ Naam, siku ya kwanza mtaondoa nyumbani mwenu unga uliokandwa wenye chachu, kwa sababu mtu yeyote atakayekula kitu kilichotiwa chachu kuanzia siku ya kwanza mpaka siku ya saba, ni lazima auawe kutoka katika Israeli. 16 Siku ya kwanza mtakuwa na kusanyiko takatifu, na siku ya saba, mtakuwa na kusanyiko lingine takatifu. Hampaswi kufanya kazi yoyote siku hizo.+ Mtatayarisha tu chakula kitakacholiwa na kila mtu.
17 “‘Mtaadhimisha Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu,+ kwa sababu siku hiyo, nitayatoa makundi yenu makubwa* katika nchi ya Misri. Nanyi mnapaswa kuiadhimisha siku hiyo katika vizazi vyenu vyote kwa kuwa ni sheria ya kudumu. 18 Katika mwezi wa kwanza, siku ya 14 ya mwezi huo, jioni, mnapaswa kula mikate isiyo na chachu mpaka siku ya 21 ya mwezi huo, jioni.+ 19 Kwa siku saba, unga uliokandwa ambao umetiwa chachu usipatikane ndani ya nyumba zenu, kwa sababu yeyote akila kitu kilichotiwa chachu, awe ni mgeni au mwenyeji wa nchi,+ mtu huyo lazima auawe kutoka katika kusanyiko la Israeli.+ 20 Hampaswi kula kitu chochote kilichotiwa chachu. Mtakula mikate isiyo na chachu katika nyumba zenu zote.”
21 Musa akawaita wazee wote wa Israeli+ bila kukawia na kuwaambia: “Nendeni mkachague wanyama wachanga* kwa ajili ya kila moja ya familia zenu, nanyi mchinje dhabihu ya Pasaka. 22 Kisha mtachovya tita la majani ya hisopo katika damu iliyo ndani ya beseni na kupiga kizingiti cha juu cha mlango na miimo yake miwili kwa tita hilo lenye damu; na mtu yeyote kati yenu asitoke nje ya mlango wa nyumba yake mpaka asubuhi. 23 Kisha Yehova atakapopita ili kuwapiga Wamisri na kuiona damu kwenye kizingiti cha juu cha mlango na kwenye miimo yake miwili, kwa hakika Yehova atapita juu ya mlango wenu, naye hataruhusu pigo la kifo liingie* katika nyumba zenu.+
24 “Mnapaswa kuadhimisha tukio hili kwa kuwa ni sheria ya kudumu kwenu na kwa wana wenu.+ 25 Nanyi mtakapoingia katika nchi ambayo Yehova atawapa kama alivyoahidi, mnapaswa kuadhimisha tukio hilo.+ 26 Na wana wenu watakapowauliza, ‘Mwadhimisho huu una maana gani kwenu?’+ 27 mnapaswa kuwaambia, ‘Tunamtolea Yehova dhabihu ya Pasaka, ambaye alipita juu ya nyumba za Waisraeli nchini Misri alipowapiga Wamisri, lakini akaacha nyumba zetu.’”
Kisha watu wakainama chini na kusujudu. 28 Basi Waisraeli wakaenda na kufanya kama Yehova alivyomwamuru Musa na Haruni.+ Hivyo ndivyo walivyofanya.
29 Ndipo katikati ya usiku, Yehova akamuua kila mzaliwa wa kwanza nchini Misri,+ kuanzia mzaliwa wa kwanza wa Farao aliyeketi kwenye kiti chake cha ufalme mpaka mzaliwa wa kwanza wa mateka aliyekuwa gerezani,* na kila mzaliwa wa kwanza wa mnyama.+ 30 Farao akaamka usiku huo pamoja na watumishi wake wote na Wamisri wengine wote, na kulikuwa na kilio kikubwa sana miongoni mwa Wamisri, kwa sababu hapakuwa na nyumba hata moja ambayo haikuwa na mtu aliyekufa.+ 31 Mara moja Farao akamwita Musa na Haruni+ usiku na kuwaambia: “Amkeni! Ondokeni kati ya watu wangu, ninyi wawili na Waisraeli wengine. Nendeni mkamtumikie Yehova, kama mlivyosema.+ 32 Chukueni pia kondoo wenu na ng’ombe wenu mwende zenu, kama mlivyosema.+ Lakini mnapaswa kunibariki pia.”
33 Na Wamisri wakaanza kuwahimiza Waisraeli waondoke haraka+ nchini “kwa sababu,” kama walivyosema, “sisi ni kama watu ambao tayari wamekufa!”+ 34 Basi Waisraeli wakachukua unga wao uliokandwa ambao haukuwa umetiwa chachu, pamoja na vyombo vyao vya* kukandia vikiwa vimefungwa katika nguo zao mabegani mwao. 35 Waisraeli walifanya kama Musa alivyokuwa amewaambia, wakawaomba Wamisri vito vya fedha na vya dhahabu na pia mavazi.+ 36 Yehova akawafanya Waisraeli wapate kibali machoni pa Wamisri, hivi kwamba wakawapa walichoomba, nao wakachukua mali za Wamisri.+
37 Kisha Waisraeli wakaondoka Ramesesi+ kwenda Sukothi,+ wanaume wapatao 600,000 waliotembea kwa miguu, bila kuhesabu watoto.+ 38 Pia, kundi kubwa lenye mchanganyiko wa watu*+ lilienda pamoja nao, na vilevile kondoo na ng’ombe, naam, mifugo wengi sana. 39 Wakaanza kuoka mikate ya mviringo isiyo na chachu kwa kutumia unga uliokandwa waliobeba kutoka Misri. Haukuwa umetiwa chachu kwa sababu walifukuzwa ghafla kutoka Misri hivi kwamba hawakuwa wamejitayarishia chakula chochote.+
40 Waisraeli walikuwa wameishi nchini Misri+ kwa miaka 430.+ 41 Mwishoni mwa miaka hiyo 430, siku hiyohiyo, makundi yote makubwa ya watu wa* Yehova yalitoka nchini Misri. 42 Wanapaswa kuadhimisha usiku huo kwa sababu Yehova aliwatoa nchini Misri. Watu wote wa Israeli katika vizazi vyao vyote wanapaswa kumheshimu Yehova kwa kuadhimisha usiku huo.+
43 Kisha Yehova akawaambia Musa na Haruni, “Hii ndiyo sheria ya Pasaka: Hakuna mgeni anayepaswa kuila.+ 44 Lakini ikiwa mtu yeyote ana mtumwa wa kiume aliyenunuliwa kwa pesa, unapaswa kumtahiri.+ Ndipo mtumwa huyo atakaposhiriki kuila. 45 Mhamiaji na kibarua hawataila. 46 Italiwa ndani ya nyumba moja. Hampaswi kutoa nyama yoyote nje ya nyumba, nanyi hampaswi kuvunja mfupa wowote wa mnyama wa Pasaka.+ 47 Kusanyiko lote la Israeli litasherehekea Pasaka. 48 Ikiwa mgeni anaishi pamoja nawe, naye anataka kusherehekea Pasaka ya Yehova, ni lazima kila mwanamume wa familia yake atahiriwe. Kisha anaweza kukaribia ili kuisherehekea, naye atakuwa kama mwenyeji wa nchi. Lakini mwanamume yeyote ambaye hajatahiriwa hapaswi kuila Pasaka.+ 49 Sheria ileile itafuatwa na mwenyeji na mgeni anayeishi miongoni mwenu.”+
50 Basi Waisraeli wote wakafanya kama Yehova alivyomwamuru Musa na Haruni. Hivyo ndivyo walivyofanya. 51 Siku hiyohiyo, Yehova aliwatoa Waisraeli pamoja na makundi yao makubwa* kutoka katika nchi ya Misri.
13 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Nitakasie* kila mzaliwa wa kwanza wa kiume wa Waisraeli. Mzaliwa wa kwanza wa kiume wa mwanadamu na mnyama ni wangu.”+
3 Ndipo Musa akawaambia watu: “Kumbukeni siku hii mliyotoka Misri,+ kutoka katika nyumba ya utumwa, kwa sababu kwa mkono wenye nguvu Yehova aliwatoa katika nchi hii.+ Kwa hiyo hampaswi kula kitu chochote kilichotiwa chachu. 4 Mnatoka Misri siku ya leo, mwezi wa Abibu.*+ 5 Mnapaswa kuiadhimisha siku hii katika mwezi huu, Yehova atakapowaleta katika nchi ya Wakanaani, Wahiti, Waamori, Wahivi, na Wayebusi,+ nchi aliyowaapia mababu zenu kwamba atawapa ninyi,+ nchi inayotiririka maziwa na asali.+ 6 Kwa siku saba mtakula mikate isiyo na chachu,+ na katika siku ya saba, mtamfanyia Yehova sherehe. 7 Mikate isiyo na chachu inapaswa kuliwa kwa siku hizo saba;+ nanyi msipatikane na kitu chochote kilicho na chachu+ wala unga wowote uliokandwa uliotiwa chachu katika eneo lenu lote.* 8 Na siku hiyo unapaswa kumwambia mwanao, ‘Ni kwa sababu ya mambo ambayo Yehova alinitendea nilipotoka Misri.’+ 9 Nayo itakuwa ishara mkononi mwako na ukumbusho kwenye paji la uso wako,*+ ili sheria ya Yehova iwe kinywani mwako, kwa sababu kwa mkono wenye nguvu Yehova alikutoa Misri. 10 Unapaswa kuishika sheria hii kwa wakati wake uliowekwa, mwaka baada ya mwaka.+
11 “Yehova atakapokuleta katika nchi ya Wakanaani, ambayo amekuapia wewe na mababu zako kwamba atakupa,+ 12 ni lazima umtolee Yehova kila mzaliwa wa kwanza wa kiume,* na pia kila mnyama dume wa mifugo yako anayezaliwa kwanza. Wazaliwa hao wa kiume ni wa Yehova.+ 13 Kila mzaliwa wa kwanza wa punda utamkomboa kwa kondoo, na usipomkomboa, basi unapaswa kumvunja shingo. Nawe unapaswa kumkomboa kila mzaliwa wa kwanza wa kiume kati ya wanao.+
14 “Mwanao akikuuliza baadaye, ‘Jambo hili linamaanisha nini?’ basi unapaswa kumwambia, ‘Kwa mkono wenye nguvu Yehova alitutoa Misri, kutoka katika nyumba ya utumwa.+ 15 Farao alipokataa kwa ukaidi kuturuhusu tuondoke,+ Yehova alimuua kila mzaliwa wa kwanza nchini Misri, kuanzia mzaliwa wa kwanza wa mwanadamu mpaka mzaliwa wa kwanza wa mnyama.+ Ndiyo sababu ninamtolea Yehova wazaliwa wote wa kwanza wa kiume* kuwa dhabihu, na kumkomboa kila mzaliwa wa kwanza kati ya wanangu.’ 16 Hiyo inapaswa kuwa ishara mkononi mwako na utepe kwenye paji la uso wako,*+ kwa sababu kwa mkono wenye nguvu Yehova alitutoa Misri.”
17 Basi Farao alipowaruhusu Waisraeli waondoke, Mungu hakuwaongoza kufuata njia ipitayo katika nchi ya Wafilisti, ingawa ilikuwa fupi. Kwa maana Mungu alisema: “Watu hawa wakikabili vita huenda wakabadili mawazo yao na kurudi Misri.” 18 Kwa hiyo Mungu akawafanya wazunguke kupitia njia ya nyikani inayoelekea kwenye Bahari Nyekundu.+ Lakini Waisraeli waliondoka katika nchi ya Misri wakiwa wamejipanga kivita. 19 Pia Musa alibeba mifupa ya Yosefu, kwa sababu Yosefu alikuwa amewaapisha hivi wana wa Israeli: “Mungu hatakosa kamwe kuwakazia uangalifu, nanyi mnapaswa kuiondoa huku mifupa yangu na kwenda nayo.”+ 20 Wakaondoka Sukothi na kupiga kambi Ethamu, ukingoni mwa nyika.
21 Sasa Yehova alikuwa akiwatangulia mchana katika nguzo ya wingu ili awaongoze njiani,+ na wakati wa usiku katika nguzo ya moto ili awape nuru, waweze kusafiri mchana na usiku.+ 22 Ile nguzo ya wingu haikuwa ikiondoka mbele ya watu wakati wa mchana, wala nguzo ya moto wakati wa usiku.+
14 Sasa Yehova akamwambia Musa: 2 “Waambie Waisraeli kwamba wanapaswa kurudi na kupiga kambi mbele ya Pihahirothi, kati ya Migdoli na bahari, mbele ya Baal-sefoni.+ Mtapiga kambi mbele yake kando ya bahari. 3 Kisha Farao atasema hivi kuhusu Waisraeli, ‘Wanatangatanga nchini kwa sababu wamechanganyikiwa. Wamepotea nyikani.’ 4 Nitauacha moyo wa Farao uwe mkaidi,+ naye atawafuatia, nami nitajipatia utukufu kupitia Farao na jeshi lake lote;+ na Wamisri watajua kwa hakika kwamba mimi ni Yehova.”+ Basi Waisraeli wakafanya hivyo.
5 Baadaye mfalme wa Misri akajulishwa kwamba Waisraeli wamekimbia. Mara moja, Farao na watumishi wake wakabadili nia kuwahusu Waisraeli,+ wakasema: “Kwa nini tulifanya hivyo na kuwaruhusu Waisraeli waondoke, wasiwe watumwa wetu?” 6 Kwa hiyo akatayarisha magari yake ya vita, akaenda pamoja na watu wake.+ 7 Akachukua magari 600 ya vita yaliyo bora na magari mengine yote ya vita nchini Misri, na kila gari lilikuwa na mashujaa. 8 Kwa hiyo Yehova akauacha moyo wa Farao mfalme wa Misri uwe mkaidi, naye akawafuatia Waisraeli, ambao walikuwa wakienda zao kwa ujasiri.*+ 9 Wamisri wakawafuatia,+ na farasi wote wa magari ya vita ya Farao na askari wake wapanda farasi na jeshi lake lilikuwa likiwakaribia Waisraeli walipokuwa wamepiga kambi kando ya bahari, karibu na Pihahirothi, mbele ya Baal-sefoni.
10 Farao alipokaribia, Waisraeli waliinua macho yao na kuwaona Wamisri wakiwafuatia. Waisraeli wakaogopa sana na kuanza kumlilia Yehova.+ 11 Wakamwambia Musa: “Je, ni kwa sababu hakuna makaburi huko Misri ndiyo sababu umetuleta hapa tufie nyikani?+ Ni jambo gani hili ulilotutendea kwa kututoa Misri? 12 Je, hili silo jambo tulilokuambia nchini Misri tuliposema, ‘Achana nasi, ili tuwatumikie Wamisri’? Kwa maana ni afadhali kwetu kuwatumikia Wamisri kuliko kufia nyikani.”+ 13 Ndipo Musa akawaambia watu: “Msiogope.+ Simameni imara muone jinsi Yehova atakavyowaokoa leo.+ Kwa maana Wamisri mnaowaona leo, hamtawaona tena kamwe.+ 14 Yehova mwenyewe atawapigania ninyi,+ nanyi mtakaa kimya.”
15 Sasa Yehova akamwambia Musa: “Kwa nini unaendelea kunililia? Waambie Waisraeli wavunje kambi. 16 Nawe inua fimbo yako na kuunyoosha mkono wako juu ya bahari na kuigawanya, ili Waisraeli wapite kwenye nchi kavu katikati ya bahari. 17 Nami ninaiacha mioyo ya Wamisri iwe mikaidi, ili waingie humo wakiwafuatia; kwa hiyo nitajipatia utukufu kupitia Farao na jeshi lake lote, magari yake ya vita, na askari wake wapanda farasi.+ 18 Na Wamisri watajua kwa hakika kwamba mimi ni Yehova nitakapojipatia utukufu kupitia Farao, magari yake ya vita, na askari wake wapanda farasi.”+
19 Ndipo malaika wa Mungu wa kweli+ aliyekuwa akitangulia kambi ya Waisraeli akaondoka na kurudi nyuma yao, nayo nguzo ya wingu iliyokuwa mbele yao ikarudi nyuma na kusimama nyuma yao.+ 20 Kwa hiyo ikaja kati ya kambi ya Wamisri na kambi ya Waisraeli.+ Upande mmoja, wingu hilo lilikuwa giza. Upande mwingine, uliangaza usiku.+ Hivyo, kambi ya Wamisri haikuikaribia kambi ya Waisraeli usiku kucha.
21 Sasa Musa akaunyoosha mkono wake juu ya bahari;+ naye Yehova akaisukuma bahari nyuma usiku kucha kwa upepo wenye nguvu wa mashariki, maji yakagawanyika,+ kukawa na nchi kavu+ katikati ya bahari. 22 Kwa hiyo Waisraeli wakapita kwenye nchi kavu katikati ya bahari,+ huku maji yakisimama kama ukuta upande wao wa kulia na wa kushoto.+ 23 Wamisri wakawafuatia; farasi wote wa Farao, magari yake ya vita, na askari wake wapanda farasi wakaanza kuwafuatia katikati ya bahari.+ 24 Wakati wa kesha la asubuhi,* Yehova alitazama kambi ya Wamisri kutoka kwenye ile nguzo ya moto na wingu,+ naye akaivuruga kambi ya Wamisri. 25 Alikuwa akiyang’oa magurudumu ya magari yao ya vita hivi kwamba waliyaendesha kwa shida, na Wamisri walikuwa wakisema: “Na tuwakimbie Waisraeli tusiwakaribie kamwe, kwa sababu Yehova anawapigania dhidi ya Wamisri.”+
26 Ndipo Yehova akamwambia Musa: “Unyooshe mkono wako juu ya bahari ili maji yarudi na kuwafunika Wamisri, magari yao ya vita, na askari wao wapanda farasi.” 27 Mara moja Musa akaunyoosha mkono wake juu ya bahari, na asubuhi ilipokuwa ikikaribia, bahari ikarudia hali yake ya kawaida. Wamisri walipokuwa wakiikimbia bahari, Yehova akawakung’uta Wamisri katikati ya bahari.+ 28 Maji yaliyokuwa yakirudi yalifunika magari ya vita na askari wapanda farasi na wanajeshi wote wa Farao waliokuwa wameingia baharini kuwafuatia.+ Hakuna hata mmoja wao aliyeokoka.+
29 Lakini Waisraeli walitembea kwenye nchi kavu katikati ya bahari,+ na maji yalisimama kama ukuta upande wao wa kulia na wa kushoto.+ 30 Kwa hiyo Yehova akawaokoa Waisraeli siku hiyo kutoka mikononi mwa Wamisri,+ nao Waisraeli wakawaona Wamisri wakiwa wamekufa kwenye ufuo wa bahari. 31 Pia Waisraeli waliona nguvu nyingi ambazo* Yehova alidhihirisha dhidi ya Wamisri, basi watu wakaanza kumwogopa Yehova na kuwa na imani katika Yehova na Musa mtumishi wake.+
15 Wakati huo Musa na Waisraeli wakamwimbia Yehova wimbo huu:+
“Acheni nimwimbie Yehova, kwa maana amekwezwa sana.+
Farasi na mpandaji wake amewavurumisha baharini.+
2 Nguvu zangu na uwezo wangu ni Yah,* kwa maana amekuwa wokovu wangu.+
Huyu ni Mungu wangu, nitamsifu;+ Mungu wa baba yangu,+ nitamkweza.+
3 Yehova ni shujaa mwenye nguvu.+ Yehova ndilo jina lake.+
4 Ametupa baharini magari ya vita ya Farao na jeshi lake,+
Na mashujaa wake bora kabisa wamezama katika Bahari Nyekundu.+
5 Mawimbi makubwa yaliwafunika; wakazama vilindini kama jiwe.+
6 Mkono wako wa kuume, Ee Yehova, una nguvu nyingi;+
Mkono wako wa kuume, Ee Yehova, unaweza kumvunjavunja adui.
7 Katika fahari yako kuu unaweza kuwaangusha chini wale wanaoinuka juu dhidi yako;+
Unaituma hasira yako inayowaka, nayo inawala kama majani makavu.
8 Kwa pumzi moja kutoka katika mianzi ya pua yako maji yalikusanyika pamoja;
Yalisimama tuli, yakazuia mafuriko;
Mawimbi makubwa yaligandamana katikati ya bahari.
9 Adui alisema, ‘Nitawafuatia! Nitawafikia!
Nitagawanya nyara mpaka nitakapotosheka!
Nitauchomoa upanga wangu! Mkono wangu utawatiisha!’+
11 Ni nani kati ya miungu aliye kama wewe, Ee Yehova?+
Ni nani aliye kama wewe, unayejidhihirisha mwenyewe kuwa mkuu katika utakatifu?+
Wewe unayestahili kuogopwa kwa nyimbo za sifa, Wewe unayetenda mambo yanayostaajabisha.+
12 Uliunyoosha mkono wako wa kuume, dunia ikawameza kabisa.+
13 Kwa upendo wako mshikamanifu umewaongoza watu uliowakomboa;+
Kwa nguvu zako utawaongoza kwenye makao yako matakatifu.
Wakaaji wote wa Kanaani watavunjika moyo.+
16 Watashikwa na woga na hofu.+
Kwa sababu ya ukuu wa mkono wako watatulia kama jiwe
Mpaka watu wako watakapopita, Ee Yehova,
17 Utawaleta na kuwapanda kwenye mlima wa urithi wako,+
Mahali pa kudumu ulipotayarisha pawe makao yako, Ee Yehova,
Mahali patakatifu, Ee Yehova, ambapo umepajenga imara kwa mikono yako.
18 Yehova atatawala akiwa mfalme milele na milele.+
19 Farasi wa Farao na magari yake ya vita na askari wake wapanda farasi walipoingia baharini,+
Ndipo Yehova alipoyarudisha maji ya bahari yakawafunika,+
Lakini Waisraeli walitembea kwenye nchi kavu katikati ya bahari.”+
20 Kisha nabii Miriamu, dada ya Haruni, akachukua tari, na wanawake wote wakamfuata wakiwa na matari yao wakicheza dansi. 21 Miriamu akaimba hivi akiwaitikia wanaume:
“Mwimbieni Yehova, kwa maana amekwezwa sana.+
Farasi na mpandaji wake amewavurumisha baharini.”+
22 Baadaye Musa akawaongoza Waisraeli kutoka katika Bahari Nyekundu, wakaenda katika nyika ya Shuri na kusafiri kwa siku tatu nyikani, lakini hawakupata maji. 23 Wakafika Mara,*+ lakini hawakuweza kunywa maji ya Mara kwa sababu yalikuwa machungu. Ndiyo sababu alipaita mahali hapo Mara. 24 Basi watu wakaanza kumnung’unikia Musa,+ wakisema: “Tutakunywa nini?” 25 Musa akamlilia Yehova,+ naye Yehova akamwelekeza kwenye mti fulani. Alipoutupa ndani ya maji hayo, yakawa matamu.
Huko Mungu akawawekea sharti na msingi wa hukumu, na huko Mungu akawajaribu.+ 26 Alisema: “Ikiwa mtaisikiliza kwa makini sauti yangu mimi, Yehova Mungu wenu na kufanya yaliyo sawa machoni pangu na kusikiliza kwa makini amri zangu na kushika masharti yangu yote,+ sitawaletea ugonjwa wowote ambao niliwaletea Wamisri,+ kwa sababu mimi, Yehova, ninawaponya.”+
27 Baada ya hapo wakafika Elimu, mahali palipokuwa na chemchemi 12 za maji na mitende 70. Kwa hiyo wakapiga kambi hapo kando ya maji.
16 Baada ya kutoka Elimu, hatimaye kusanyiko lote la Waisraeli likafika katika nyika ya Sini,+ kati ya Elimu na Sinai, siku ya 15 ya mwezi wa pili baada ya kutoka katika nchi ya Misri.
2 Kisha kusanyiko lote la Waisraeli likaanza kuwanung’unikia Musa na Haruni nyikani.+ 3 Waisraeli waliendelea kuwanung’unikia wakisema: “Laiti mkono wa Yehova ungetuua katika nchi ya Misri tulipokuwa tukiketi kando ya vyungu vya nyama,+ tulipokuwa tukila na kushiba mikate. Sasa mmetutoa huko na kutuleta katika nyika hii ili kuliua kusanyiko hili lote kwa njaa kali.”+
4 Ndipo Yehova akamwambia Musa: “Tazama, ninawanyeshea mkate kutoka mbinguni,+ na kila mtu anapaswa kwenda kukusanya kiasi kinachomtosha siku baada ya siku,+ ili niwajaribu nione kama watafuata sheria yangu au la.+ 5 Lakini siku ya sita+ wanapotayarisha kiasi walichokusanya, kinapaswa kuwa mara mbili ya kiasi wanachokusanya kila siku, siku nyinginezo.”+
6 Kwa hiyo Musa na Haruni wakawaambia Waisraeli wote: “Jioni mtajua kwa hakika kwamba Yehova ndiye aliyewatoa ninyi nchini Misri.+ 7 Asubuhi mtauona utukufu wa Yehova, kwa sababu Yehova amesikia manung’uniko yenu dhidi yake. Sisi ni nani hivi kwamba mnung’unike dhidi yetu?” 8 Musa akaendelea kusema: “Yehova atakapowapa nyama ya kula jioni na mikate mtakayokula asubuhi na kushiba, mtajua kwamba Yehova amesikia manung’uniko yenu mnayonung’unika dhidi yake. Lakini sisi ni nani? Hamnung’uniki dhidi yetu, bali dhidi ya Yehova.”+
9 Kisha Musa akamwambia Haruni: “Liambie hivi kusanyiko lote la Waisraeli, ‘Karibieni mbele za Yehova, kwa maana amesikia manung’uniko yenu.’”+ 10 Mara tu Haruni alipomaliza kuzungumza na kusanyiko lote la Waisraeli, waligeuka na kutazama nyikani, na tazama! utukufu wa Yehova ukatokea katika lile wingu.+
11 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 12 “Nimesikia manung’uniko ya Waisraeli.+ Waambie hivi: ‘Jioni kabla ya giza kuingia* mtakula nyama, na asubuhi mtashiba mikate,+ nanyi mtajua kwa hakika kwamba mimi ni Yehova Mungu wenu.’”+
13 Basi jioni hiyo kware wakaja na kufunika kambi,+ na asubuhi utando wa umande ulizunguka kambi yote. 14 Utando huo wa umande ulipotoweka, kitu laini, kinachovunjikavunjika,+ kitu laini kama theluji, kilienea kwenye ardhi nyikani. 15 Waisraeli walipokiona, walianza kuulizana: “Ni nini hiki?” kwa maana hawakujua kilikuwa nini. Musa akawaambia: “Ni mkate ambao Yehova amewapa uwe chakula chenu.+ 16 Yehova ameamuru hivi: ‘Kila mtu anapaswa kukusanya kiasi anachoweza kula. Kila mmoja wenu atachukua kiasi cha omeri moja*+ kwa ajili ya kila mtu aliye katika hema lake.’” 17 Waisraeli wakaanza kukusanya; baadhi yao walikusanya zaidi na wengine wakakusanya kidogo. 18 Walipopima kwa omeri, yule aliyekusanya zaidi hakuwa na ziada na yule aliyekusanya kidogo hakupungukiwa.+ Kila mmoja alikusanya kiasi alichoweza kula.
19 Kisha Musa akawaambia: “Hakuna yeyote anayepaswa kuubakiza mkate huo mpaka asubuhi.”+ 20 Lakini hawakumsikiliza Musa. Baadhi yao walipoubakiza mpaka asubuhi, ulipata mabuu na kunuka, hivyo Musa akawakasirikia sana. 21 Waliuokota asubuhi baada ya asubuhi, kila mtu kulingana na kiasi alichoweza kula. Jua lilipokuwa kali, uliyeyuka.
22 Siku ya sita, waliokota kiasi mara mbili,+ vipimo viwili vya omeri kwa kila mtu. Kwa hiyo wakuu wote wa kusanyiko wakaja na kumwambia Musa jambo hilo. 23 Musa akawaambia: “Hivyo ndivyo alivyosema Yehova. Kesho kutakuwa na pumziko kamili,* sabato takatifu kwa Yehova.+ Okeni mnachohitaji kuoka, na chemsheni mnachohitaji kuchemsha;+ kisha chochote kitakachobaki mkihifadhi mpaka asubuhi.” 24 Basi wakakihifadhi mpaka asubuhi, kama Musa alivyowaamuru, nacho hakikunuka wala kuwa na mabuu. 25 Kisha Musa akasema: “Kuleni chakula hicho leo, kwa sababu leo ni sabato kwa Yehova. Leo hamtakipata kwenye ardhi. 26 Mtakiokota kwa siku sita, lakini siku ya saba ni Sabato,+ hakitakuwepo.” 27 Lakini baadhi ya watu walienda kukiokota siku ya saba, lakini hawakupata chochote.
28 Kwa hiyo Yehova akamwambia Musa: “Mtakataa kushika amri na sheria zangu mpaka lini?+ 29 Zingatieni kwamba mimi, Yehova, nimewapa Sabato.+ Ndiyo sababu katika siku ya sita ninawapa mkate wa siku mbili. Kila mtu anapaswa kukaa mahali alipo; hakuna yeyote anayepaswa kutoka kwake siku ya saba.” 30 Kwa hiyo watu wakaadhimisha Sabato* siku ya saba.+
31 Watu wa nyumba ya Israeli waliuita mkate huo “mana.”* Ulikuwa mweupe kama mbegu za mgiligilani, na ladha yake ilikuwa kama ya keki bapa zenye asali.+ 32 Kisha Musa akasema: “Yehova ameamuru hivi: ‘Jazeni mkate huo katika kipimo cha omeri ili uwe kitu kitakachohifadhiwa katika vizazi vyenu vyote,+ ili watoto wenu waone mkate niliowapa mle nyikani nilipokuwa nikiwatoa katika nchi ya Misri.’” 33 Basi Musa akamwambia Haruni: “Chukua mtungi na kutia humo omeri moja ya mana, nawe uiweke mbele za Yehova ili iwe kitu kitakachohifadhiwa katika vizazi vyenu vyote.”+ 34 Haruni akafanya kama Yehova alivyomwamuru Musa, akaiweka mbele ya sanduku la Ushahidi*+ ili ihifadhiwe. 35 Waisraeli walikula mana kwa miaka 40,+ mpaka walipofika katika nchi iliyokaliwa na watu.+ Walikula mana mpaka walipofika mpakani mwa nchi ya Kanaani.+ 36 Sasa omeri ni sehemu ya kumi ya kipimo cha efa.*
17 Kusanyiko lote la Waisraeli likaondoka katika nyika ya Sini+ hatua kwa hatua kama Yehova alivyoagiza,+ wakapiga kambi Refidimu.+ Lakini watu hawakuwa na maji ya kunywa.
2 Basi watu wakaanza kugombana na Musa+ wakisema: “Tupe maji ya kunywa!” Lakini Musa akawauliza: “Kwa nini mnagombana nami? Kwa nini mnaendelea kumjaribu Yehova?”+ 3 Lakini watu walikuwa na kiu sana mahali hapo, nao wakaendelea kumnung’unikia Musa+ wakisema: “Kwa nini umetupandisha kutoka Misri ili kutuua kwa kiu sisi na wana wetu na mifugo yetu?” 4 Mwishowe Musa akamlilia Yehova akisema: “Nifanye nini na watu hawa? Hivi punde watanipiga mawe!”
5 Kisha Yehova akamwambia Musa: “Nenda mbele ya watu, wachukue wazee kadhaa wa Israeli na fimbo yako uliyotumia kupiga maji ya Mto Nile.+ Ibebe mkononi mwako na uendelee kutembea. 6 Tazama! Nitakuwa nimesimama mbele yako kwenye mwamba huko Horebu. Unapaswa kuupiga mwamba huo, na maji yatatoka ndani yake, kisha watu watayanywa.”+ Musa akafanya hivyo mbele ya wazee wa Israeli. 7 Basi akapaita mahali hapo Masa*+ na Meriba,*+ kwa sababu ya ugomvi wa Waisraeli na kwa sababu walimjaribu+ Yehova kwa kusema: “Je, Yehova yuko katikati yetu au la?”
8 Kisha Waamaleki+ wakaja na kupigana na Waisraeli huko Refidimu.+ 9 Ndipo Musa akamwambia Yoshua:+ “Tuchagulie wanaume wakapigane na Waamaleki. Kesho nitasimama juu ya kilima, nikiwa na fimbo ya Mungu wa kweli mkononi mwangu.” 10 Basi Yoshua akafanya kama Musa alivyomwambia,+ akapigana na Waamaleki. Naye Musa, Haruni, na Huru+ wakapanda juu ya kilima.
11 Wakati wote ambapo Musa aliinua mikono yake, Waisraeli walishinda, lakini mara tu alipoishusha mikono yake, Waamaleki walishinda. 12 Mikono ya Musa ilipochoka, walichukua jiwe wakaliweka chini yake, akaketi juu ya jiwe hilo. Kisha Haruni na Huru, mmoja upande huu na mwingine upande mwingine, wakaitegemeza mikono yake, hivi kwamba mikono yake ikabaki imara mpaka jua lilipotua. 13 Kwa hiyo Yoshua akawashinda kwa upanga Waamaleki na watu walioshirikiana nao.+
14 Sasa Yehova akamwambia Musa: “Andika jambo hili katika kitabu liwe ukumbusho,* na uliseme tena kwa Yoshua: ‘Nitawaangamiza kabisa Waamaleki kutoka chini ya mbingu, nao hawatakumbukwa tena.’”+ 15 Kisha Musa akajenga madhabahu na kuiita Yehova-nisi,* 16 na kusema: “Kwa sababu mkono wa Waamaleki unapinga kiti cha ufalme cha Yah,+ Yehova atapigana vita na Waamaleki kizazi baada ya kizazi.”+
18 Sasa Yethro kuhani wa Midiani, baba mkwe wa Musa,+ akasikia mambo yote ambayo Mungu alikuwa amemtendea Musa na watu wake Waisraeli, jinsi Yehova alivyowatoa Waisraeli nchini Misri.+ 2 Yethro, baba mkwe wa Musa, alikuwa amemchukua Sipora mke wa Musa ili amtunze, Sipora aliporudishwa 3 pamoja na wanawe wawili.+ Mwana mmoja aliitwa Gershomu,*+ kwa sababu Musa alisema, “Nimekuwa mkaaji mgeni katika nchi ya kigeni,” 4 na yule mwingine aliitwa Eliezeri,* kwa sababu Musa alisema, “Mungu wa baba yangu ni msaidizi wangu, aliyeniokoa kutokana na upanga wa Farao.”+
5 Basi Yethro, baba mkwe wa Musa, pamoja na wana na mke wa Musa, wakaja kwa Musa nyikani ambako alikuwa amepiga kambi karibu na mlima wa Mungu wa kweli.+ 6 Kisha akatuma ujumbe huu kwa Musa: “Mimi, Yethro, baba mkwe wako,+ naja kwako pamoja na mke wako na wanawe wawili.” 7 Mara moja Musa akaenda kumpokea baba mkwe wake, akainama chini na kumbusu. Wakajuliana hali, kisha wakaingia hemani.
8 Musa akamsimulia baba mkwe wake mambo yote ambayo Yehova alikuwa amemtendea Farao na Wamisri kwa ajili ya Waisraeli,+ matatizo yote waliyopata safarini,+ na jinsi Yehova alivyowaokoa. 9 Yethro akashangilia kwa sababu ya mambo yote mema ambayo Yehova aliwatendea Waisraeli kwa kuwaokoa kutoka Misri.* 10 Kisha Yethro akasema: “Yehova na asifiwe, aliyekuokoa kutoka Misri na kutoka kwa Farao, na kuwaokoa Waisraeli kutoka mikononi mwa Wamisri. 11 Sasa ninajua kwamba Yehova ni mkuu kuliko miungu mingine yote,+ kwa sababu ya mambo aliyowafanyia wale waliowatendea watu wake kwa kiburi.” 12 Kisha Yethro, baba mkwe wa Musa, akaleta dhabihu ya kuteketezwa na matoleo kwa ajili ya Mungu, na Haruni na wazee wote wa Israeli wakaja kula chakula pamoja na baba mkwe wa Musa, mbele za Mungu wa kweli.
13 Siku iliyofuata, Musa akaketi kama kawaida ili kusikiliza kesi za watu, na watu wakaendelea kuja na kusimama mbele ya Musa tangu asubuhi mpaka jioni. 14 Baba mkwe wake alipoona mambo yote ambayo Musa alikuwa akiwafanyia watu, akamuuliza: “Ni nini hiki unachowafanyia watu? Kwa nini unaketi hapa peke yako huku watu wote wakisimama mbele yako tangu asubuhi mpaka jioni?” 15 Musa akamwambia baba mkwe wake: “Ni kwa sababu watu wanaendelea kuja kwangu kutafuta mwongozo kutoka kwa Mungu. 16 Wakiwa na kesi, wanaileta kwangu, nami lazima niamue kesi yao, na kuwajulisha maamuzi ya Mungu wa kweli na sheria zake.”+
17 Baba mkwe wa Musa akamwambia: “Jambo unalofanya si zuri. 18 Kwa hakika utachoka, wewe na watu hawa walio pamoja nawe, kwa sababu mzigo huu ni mkubwa sana kwako na huwezi kuubeba peke yako. 19 Sasa nisikilize. Nitakupa ushauri, na Mungu atakuwa pamoja nawe.+ Wewe uwe mwakilishi wa watu mbele za Mungu wa kweli,+ nawe lazima uwasilishe kesi zao mbele za Mungu wa kweli.+ 20 Unapaswa kuwaonya kwa kuwafundisha masharti na sheria,+ na uwajulishe njia wanayopaswa kufuata na kazi wanayopaswa kufanya. 21 Lakini unapaswa kuchagua miongoni mwa watu, wanaume wanaostahili,+ wanaomwogopa Mungu, wanaume wanaotegemeka, wanaochukia faida isiyo ya haki,+ nawe uwaweke kuwa wakuu wa maelfu, wakuu wa mamia, wakuu wa hamsini, na wakuu wa makumi.+ 22 Watakuwa waamuzi wa watu kunapokuwa na kesi,* nao watakuletea kila kesi iliyo ngumu,+ lakini wao wataamua kila kesi ambayo ni ndogo. Jirahisishie mzigo huu kwa kuwaruhusu wakusaidie kuubeba.+ 23 Ukifanya hivyo, na iwe ndivyo Mungu anavyokuamuru, utaweza kustahimili mkazo huu, na kila mtu atarudi nyumbani akiwa ameridhika.”
24 Mara moja Musa akamsikiliza baba mkwe wake na kufanya yote aliyosema. 25 Musa akachagua wanaume wanaostahili miongoni mwa Waisraeli wote na kuwaweka kuwa viongozi wa watu, kuwa wakuu wa maelfu, wakuu wa mamia, wakuu wa hamsini, na wakuu wa makumi. 26 Kwa hiyo waliamua kesi walizoletewa na watu. Kesi ngumu walimletea Musa,+ lakini waliamua kila kesi ndogo. 27 Kisha Musa akamuaga baba mkwe wake,+ naye baba mkwe wake akashika njia na kurudi katika nchi yake.
19 Katika mwezi wa tatu baada ya Waisraeli kutoka nchini Misri, siku ileile, walifika katika nyika ya Sinai. 2 Waliondoka Refidimu+ wakafika katika nyika ya Sinai na kupiga kambi nyikani. Waisraeli walipiga kambi huko mbele ya mlima.+
3 Kisha Musa akapanda mlimani kwa Mungu wa kweli, naye Yehova akamwita kutoka mlimani,+ akamwambia: “Hivi ndivyo utakavyoiambia nyumba ya Yakobo na kuwaambia Waisraeli, 4 ‘Mmejionea wenyewe mambo niliyowatendea Wamisri,+ ili niwabebe juu ya mabawa ya tai na kuwaleta kwangu.+ 5 Sasa ikiwa mtaitii kabisa sauti yangu na kushika agano langu, hakika mtakuwa mali yangu ya pekee* kati ya mataifa yote,+ kwa maana dunia yote ni mali yangu.+ 6 Mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani na taifa takatifu.’+ Hayo ndiyo maneno utakayowaambia Waisraeli.”
7 Basi Musa akaenda na kuwaita wazee wote wa Waisraeli na kuwaambia maneno hayo yote ambayo Yehova alikuwa amemwamuru.+ 8 Kisha watu wote wakasema pamoja: “Mambo yote ambayo Yehova amesema, tuko tayari kufanya.”+ Mara moja Musa akamwambia Yehova maneno hayo ambayo watu walisema. 9 Na Yehova akamwambia Musa: “Tazama! nitakujia katika wingu lenye giza, ili watu wasikie ninapozungumza nawe na ili wakuamini wewe pia sikuzote.” Kisha Musa akamwambia Yehova maneno ambayo watu walisema.
10 Halafu Yehova akamwambia Musa: “Nenda uwatakase watu leo na kesho, nao lazima wafue nguo zao. 11 Nao lazima wawe tayari kwa ajili ya siku ya tatu, kwa sababu katika siku ya tatu mimi Yehova nitashuka juu ya Mlima Sinai mbele ya watu wote. 12 Ni lazima uwawekee watu mipaka kuzunguka mlima huu na uwaambie, ‘Jihadharini msipande mlimani wala kugusa ukingo wake. Yeyote atakayeugusa mlima huu hakika atauawa. 13 Mkono wa yeyote usimguse, atapigwa mawe au kuchomwa kwa silaha.* Awe ni mnyama au mwanadamu, hataishi.’+ Lakini pembe ya kondoo dume+ ikipigwa watu wanaweza kuukaribia mlima.”
14 Kisha Musa akashuka kutoka mlimani, akaenda kwa watu, akaanza kuwatakasa, nao wakafua nguo zao.+ 15 Akawaambia: “Jitayarisheni kwa ajili ya siku ya tatu. Msifanye ngono.”*
16 Asubuhi, siku ya tatu, kulikuwa na ngurumo na radi, na kulikuwa na wingu zito+ mlimani na sauti kubwa sana ya pembe, na watu wote kambini wakaanza kutetemeka.+ 17 Sasa Musa akawatoa watu nje ya kambi ili wakutane na Mungu wa kweli, nao wakasimama mahali pao chini ya mlima. 18 Mlima Sinai ulifuka moshi kila mahali, kwa sababu Yehova alishuka juu yake katika moto;+ na moshi huo ulikuwa ukipaa kama moshi wa tanuru,* na mlima wote ulikuwa ukitetemeka kwa nguvu sana.+ 19 Sauti ya pembe ilipozidi kuongezeka zaidi na zaidi, Musa akaongea, na sauti ya Mungu wa kweli ikamjibu.
20 Kwa hiyo Yehova akashuka juu ya kilele cha Mlima Sinai. Kisha Yehova akamwita Musa apande juu mlimani, naye Musa akapanda mlimani.+ 21 Sasa Yehova akamwambia Musa: “Shuka chini ukawaonye watu wasijaribu kuvuka mpaka kuja kunitazama mimi, Yehova, la sivyo wengi wao wataangamia. 22 Nao makuhani wanaonikaribia mimi Yehova kwa ukawaida, wanapaswa kujitakasa, ili mimi, Yehova, nisiwaangamize.”+ 23 Basi Musa akamwambia Yehova: “Watu hawawezi kuukaribia Mlima Sinai kwa sababu tayari ulituonya, uliponiambia, ‘Weka mipaka kuzunguka mlima huu, ili uwe mtakatifu.’”+ 24 Hata hivyo, Yehova akamwambia: “Nenda, shuka chini, na urudi juu, wewe pamoja na Haruni, lakini usiwaruhusu makuhani na watu wavuke mpaka na kunikaribia mimi Yehova, ili nisiwaangamize.”+ 25 Basi Musa akashuka na kuwaambia watu maneno hayo.
20 Kisha Mungu akasema maneno haya yote:+
2 “Mimi ni Yehova Mungu wako, niliyekutoa katika nchi ya Misri, kutoka katika nyumba ya utumwa.+ 3 Usiwe na miungu mingine yoyote ila mimi.*+
4 “Usijitengenezee sanamu ya kuchongwa au mfano wa* kitu chochote kilicho juu mbinguni au kilicho chini duniani au kilicho ndani ya maji chini ya dunia.+ 5 Usiviinamie wala kushawishiwa kuviabudu,+ kwa sababu mimi, Yehova Mungu wako, ni Mungu ninayetaka watu waniabudu mimi peke yangu,+ nami huwaadhibu watoto kwa sababu ya makosa ya baba zao, kufikia kizazi cha tatu na kizazi cha nne cha wale wanaonichukia, 6 lakini ninawatendea kwa upendo mshikamanifu watu wanaonipenda na kushika amri zangu, kufikia kizazi cha elfu cha watu hao.+
7 “Usilitumie jina langu mimi, Yehova Mungu wako, kwa njia isiyofaa,+ kwa maana mimi, Yehova, sitakosa kumwadhibu yule anayelitumia jina langu kwa njia isiyofaa.+
8 “Ikumbuke siku ya Sabato na uione kuwa takatifu.+ 9 Fanya shughuli na kazi zako zote kwa siku sita,+ 10 lakini siku ya saba ni sabato kwa Yehova Mungu wako. Usifanye kazi yoyote, wewe wala mwana wako wala binti yako wala mtumwa wako wala kijakazi wako wala mnyama wako wa kufugwa wala mgeni aliye katika makazi* yako.+ 11 Kwa maana kwa siku sita mimi, Yehova, niliumba mbingu na dunia, bahari, na vitu vyote vilivyomo, nami nikaanza kupumzika siku ya saba.+ Ndiyo sababu mimi Yehova niliibariki siku ya Sabato na kuifanya kuwa takatifu.
12 “Mheshimu baba yako na mama yako+ ili uishi muda mrefu katika nchi ambayo mimi Yehova Mungu wako ninakupa.+
16 “Usitoe ushahidi wa uwongo dhidi ya jirani yako.+
17 “Usiitamani nyumba ya jirani yako. Usimtamani mke wa jirani yako+ wala mtumwa wake wala kijakazi wake wala ng’ombe dume wake wala punda wake wala kitu chochote cha jirani yako.”+
18 Sasa watu wote walikuwa wakishuhudia ngurumo na radi, sauti ya pembe, na mlima ukifuka moshi; na walipoona mambo hayo walitetemeka na kusimama mbali.+ 19 Basi wakamwambia Musa: “Wewe ongea nasi, tutasikiliza, lakini Mungu asiongee nasi tusije tukafa.”+ 20 Kwa hiyo Musa akawaambia watu: “Msiogope, kwa sababu Mungu wa kweli amekuja kuwajaribu,+ ili mwendelee kumwogopa, msitende dhambi.”+ 21 Kwa hiyo watu wakaendelea kusimama mbali, lakini Musa akalikaribia lile wingu jeusi mahali alipokuwa Mungu wa kweli.+
22 Kisha Yehova akamwambia Musa: “Hivi ndivyo utakavyowaambia Waisraeli, ‘Mmejionea wenyewe kwamba nimezungumza nanyi kutoka mbinguni.+ 23 Msijitengenezee miungu ya fedha na kuiabudu huku mkiniabudu mimi, wala msijitengenezee miungu ya dhahabu.+ 24 Mtanijengea madhabahu ya udongo, na juu yake mtanitolea dhabihu zenu za kuteketezwa, dhabihu zenu za ushirika,* kondoo, mbuzi, na ng’ombe wenu. Mahali popote nitakapochagua jina langu likumbukwe,+ nitawajia, nami nitawabariki. 25 Ikiwa mtanijengea madhabahu ya mawe, msiijenge kwa mawe yaliyokatwa kwa vifaa.*+ Kwa maana mkiyachonga kwa tindo, mtaitia madhabahu hiyo unajisi. 26 Nanyi msipande madhabahu yangu kwa ngazi, ili sehemu zenu za siri zisionekane* juu yake.’
21 “Hizi ndizo sheria utakazowapa* Waisraeli:+
2 “Ukimnunua mtumwa Mwebrania,+ atakuwa mtumwa kwa miaka sita, lakini mwaka wa saba, utamweka huru, naye hatalipa chochote.+ 3 Ikiwa alikuja peke yake, ataondoka peke yake. Ikiwa ana mke, basi mke wake anapaswa kuondoka naye. 4 Ikiwa bwana wake atampa mke, na mke huyo amzalie wana au mabinti, mke huyo na watoto wake watakuwa mali ya bwana wake, na mtumwa huyo ataondoka peke yake.+ 5 Lakini mtumwa huyo akisisitiza hivi: ‘Nampenda bwana wangu, mke wangu, na wanangu; sitaki kuachiliwa huru,’+ 6 ni lazima bwana wake amlete mbele za Mungu wa kweli. Kisha bwana huyo atamleta kwenye mlango au kwenye mwimo wa mlango na kulitoboa sikio lake kwa sindano, naye atakuwa mtumwa wake maisha yake yote.
7 “Mtu akimuuza binti yake kuwa mtumwa, hataondoka kama mtumwa wa kiume anavyoondoka. 8 Ikiwa bwana wake hapendezwi naye na hataki awe suria wake, lakini aamue kumuuza kwa mtu mwingine,* bwana huyo hana haki ya kumuuza kwa wageni kwa sababu amemsaliti mtumwa huyo. 9 Akimchagua awe mke wa mwanawe, anapaswa kumpa haki anazostahili kama binti yake. 10 Ikiwa ataoa mke mwingine, hapaswi kumpunguzia mke huyo wa kwanza chakula, mavazi, na haki yake ya ndoa.+ 11 Ikiwa hatampa mambo hayo matatu, basi mtumwa huyo wa kike ataondoka bila kulipa pesa zozote.
12 “Yeyote anayempiga mtu na kumuua lazima auawe.+ 13 Lakini ikiwa alimuua bila kukusudia na Mungu wa kweli akaruhusu jambo hilo litokee, basi nitawaonyesha mahali anapoweza kukimbilia.+ 14 Mtu akimkasirikia vikali mwenzake na kumuua kwa kukusudia,+ mtu huyo lazima afe hata ikiwalazimu kumwondoa kwenye madhabahu yangu.+ 15 Mtu anayempiga baba yake au mama yake lazima auawe.+
16 “Yeyote anayemteka nyara mtu mwingine+ na kumuuza au akipatikana amemzuilia,+ lazima auawe.+
17 “Yeyote anayemlaani baba yake au mama yake lazima auawe.+
18 “Hivi ndivyo mtakavyofanya wanaume wakigombana na mmoja wao ampige mwenzake kwa jiwe au ngumi* lakini asimuue bali amjeruhi hivi kwamba ashindwe kutoka kitandani: 19 Ikiwa anaweza kutoka kitandani na kutembea nje kwa kutumia fimbo, basi yule aliyempiga hataadhibiwa. Atamlipa tu fidia kwa ajili ya wakati aliopoteza alipokuwa kitandani mpaka atakapopona kabisa.
20 “Mtu akimpiga kwa fimbo mtumwa wake wa kiume au wa kike naye afie mikononi mwake, ni lazima mtumwa huyo alipiziwe kisasi.+ 21 Hata hivyo, mtumwa huyo akiendelea kuishi kwa siku moja au siku mbili, hatalipiziwa kisasi, kwa sababu alinunuliwa kwa pesa za bwana wake.
22 “Wanaume wakipambana na kumuumiza mwanamke mwenye mimba naye azae kabla ya wakati*+ lakini kifo kisitokee,* yule aliyemuumiza atalipa hasara atakayodaiwa na mume wa mwanamke huyo; naye atalipa kupitia waamuzi.+ 23 Lakini kifo kikitokea, basi ni lazima mlipe uhai kwa uhai,*+ 24 jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono, mguu kwa mguu,+ 25 alama ya moto kwa alama ya moto, jeraha kwa jeraha, pigo kwa pigo.
26 “Mtu akilipiga jicho la mtumwa wake wa kiume au jicho la mtumwa wake wa kike na kuliharibu, atamwachilia huru mtumwa huyo ili kufidia jicho lake.+ 27 Naye akimpiga na kumng’oa jino mtumwa wake wa kiume au wa kike, atamwachilia huru mtumwa huyo ili kufidia jino lake.
28 “Ng’ombe dume akimpiga pembe mwanamume au mwanamke na kumuua, ng’ombe dume huyo atauawa kwa kupigwa mawe+ na nyama yake haipaswi kuliwa; lakini mwenye ng’ombe dume huyo hataadhibiwa. 29 Lakini ikiwa ng’ombe dume alizoea kuwapiga watu pembe na mwenyewe akaonywa lakini hakumfunga, naye amuue mwanamume au mwanamke, ng’ombe dume huyo anapaswa kupigwa mawe na mwenye ng’ombe dume huyo anapaswa kuuawa pia. 30 Ikiwa atadaiwa fidia,* atalipa chochote atakachodaiwa ili kukomboa uhai wake.* 31 Ng’ombe dume huyo akimpiga pembe mtoto wa kiume au wa kike, mwenye ng’ombe dume huyo atatendewa kulingana na sheria hii. 32 Ng’ombe dume huyo akimpiga pembe mtumwa wa kiume au wa kike, mwenye ng’ombe dume huyo atamlipa bwana wa mtumwa huyo shekeli 30,* na ng’ombe dume huyo atauawa kwa kupigwa mawe.
33 “Mtu akiacha shimo wazi au akichimba shimo na kukosa kulifunika, na ng’ombe dume au punda aanguke humo, 34 mwenye shimo hilo atalipa fidia.+ Atamlipa mwenye mnyama huyo, na mnyama aliyekufa atakuwa wake. 35 Ng’ombe dume akimuumiza na kumuua ng’ombe dume wa mtu mwingine, basi watamuuza ng’ombe dume aliye hai na kugawana pesa hizo; wanapaswa pia kugawana ng’ombe aliyekufa. 36 Au ikiwa ilijulikana kwamba ng’ombe dume alizoea kupiga kwa pembe lakini mwenye ng’ombe dume huyo hakumfunga, lazima alipe ng’ombe dume kwa ng’ombe dume, kisha ng’ombe dume aliyekufa atakuwa wake.
22 “Mtu akiiba ng’ombe dume au kondoo na kumchinja au kumuuza, atalipa ng’ombe dume watano kwa ajili ya ng’ombe dume huyo na kondoo wanne kwa ajili ya kondoo huyo.+
2 (“Mwizi+ akipatikana akivunja nyumba kisha apigwe na kufa, aliyemuua hatakuwa na hatia ya damu. 3 Lakini jambo hilo likitokea baada ya jua kuchomoza, atakuwa na hatia ya damu.)
“Anapaswa kulipa. Ikiwa hana chochote, basi atauzwa ili kulipia vitu alivyoiba. 4 Kama mnyama aliyeibwa anapatikana akiwa hai mikononi mwake, awe ni ng’ombe dume au punda au kondoo, anapaswa kulipa mara mbili.
5 “Mtu yeyote akiwalisha wanyama wake katika shamba au shamba la mizabibu la mtu mwingine, atalipa kwa mazao bora ya shamba lake mwenyewe au mazao bora ya shamba lake mwenyewe la mizabibu.
6 “Moto ukiwaka na kuenea katika vichaka vya miiba na kuteketeza masuke au nafaka iliyo shambani au shamba, yule aliyewasha moto huo lazima alipie kilichoteketea.
7 “Mtu akimpa jirani yake pesa au vitu amtunzie, navyo viibwe kutoka katika nyumba ya jirani huyo, mwizi akipatikana, lazima alipe mara mbili.+ 8 Mwizi asipopatikana, mwenye nyumba ataletwa mbele za Mungu wa kweli+ ili ithibitishwe ikiwa alichukua vitu vya jirani yake au la. 9 Katika visa vyote vya kumiliki vitu isivyo halali, iwe ni ng’ombe dume, punda, kondoo, nguo, au kitu chochote kilichopotea ambacho huenda mtu akasema, ‘Hiki ni changu!’ wote wawili wataleta kesi yao mbele za Mungu wa kweli.+ Yule ambaye Mungu atasema ana hatia atamlipa jirani yake mara mbili.+
10 “Mtu akimpa jirani yake punda au ng’ombe dume au kondoo au mnyama yeyote wa kufugwa amtunzie, kisha mnyama huyo afe au alemazwe au achukuliwe bila mtu yeyote kuona, 11 yule aliyepewa mali hiyo ataapa mbele za Yehova kwamba hakuchukua mali ya jirani yake; na mwenye mali anapaswa kukubali jambo hilo. Mtu huyo hatalipa chochote.+ 12 Lakini ikiwa mnyama huyo ameibwa kutoka kwake, atamlipa mwenye mnyama huyo. 13 Ikiwa mnyama huyo aliraruliwa na mnyama wa mwituni, atamleta kama ushahidi. Hatalipia kitu kilichoraruliwa na mnyama wa mwituni.
14 “Lakini mtu yeyote akiazima mnyama kutoka kwa jirani yake, na mnyama huyo alemazwe au afe wakati mwenyewe hayupo, aliyeazima mnyama huyo lazima alipe. 15 Ikiwa mwenyewe yupo, aliyeazima hatalipa. Ikiwa mnyama huyo alikodiwa, pesa iliyolipwa ili kumkodi ndiyo itakayokuwa malipo yake.
16 “Sasa mwanamume akimtongoza bikira ambaye hajachumbiwa kisha alale naye, lazima alipe mahari ili msichana huyo awe mke wake.+ 17 Baba yake akikataa kabisa kumpa msichana huyo, mwanamume huyo atalipa kiasi cha pesa kinacholingana na mahari.
18 “Hampaswi kumwacha mwanamke mchawi aishi.+
19 “Mtu yeyote anayefanya ngono na mnyama lazima auawe.+
20 “Mtu yeyote anayetoa dhabihu kwa miungu mingine isipokuwa kwa Yehova peke yake lazima auawe.+
21 “Msimtese wala kumkandamiza mkaaji mgeni,+ kwa sababu ninyi mlikuwa wakaaji wageni katika nchi ya Misri.+
22 “Msimtese mjane wala yatima.+ 23 Mkimtesa hata kidogo, naye anililie, hakika nitasikia kilio chake;+ 24 nami nitawaka hasira, nami nitawaua kwa upanga, na wake zenu watakuwa wajane, na watoto wenu watakuwa mayatima.
25 “Ukimkopesha pesa mtu yeyote maskini miongoni mwa watu wangu, mtu anayeishi nawe, usiwe kama mtu anayemkopesha pesa.* Hupaswi kumtoza riba.+
26 “Ukichukua nguo ya jirani yako kuwa dhamana ya mkopo,*+ unapaswa kumrudishia kabla ya jua kutua. 27 Kwa sababu hiyo ndiyo nguo pekee aliyo nayo ya kujifunika, nguo ya kufunika mwili wake,* atajifunikia nini anapolala?+ Akinililia, hakika nitasikia, kwa sababu mimi ni mwenye huruma.*+
28 “Usimtukane Mungu+ wala kumlaani kiongozi* miongoni mwa watu wako.+
29 “Usisite kutoa matoleo kutoka katika mazao yako mengi na kutoka kwenye mafuriko ya mashinikizo yako.*+ Unapaswa kunipa mzaliwa wa kwanza kati ya wanao.+ 30 Hivi ndivyo utakavyofanya kuhusu ng’ombe dume wako na kondoo wako:+ Atakaa na mama yake kwa siku saba. Siku ya nane, utanipa mimi.+
31 “Mnapaswa kujithibitisha wenyewe kuwa watu watakatifu mbele zangu,+ nanyi hampaswi kula nyama ya mnyama yeyote ambaye ameraruliwa na mnyama wa mwituni.+ Mnapaswa kuwatupia mbwa nyama hiyo.
23 “Usieneze habari za uwongo.+ Usishirikiane na mtu mwovu kwa kutoa ushahidi utakaowadhuru wengine.+ 2 Usiufuate umati ili kutenda maovu, wala usipotoshe haki kwa kutoa ushahidi wa uwongo ili uunge mkono umati.* 3 Usionyeshe upendeleo katika kesi ya mtu maskini.+
4 “Ukikutana na ng’ombe dume au punda wa adui yako akitangatanga, unapaswa kumrudisha kwake.+ 5 Ukimwona punda wa mtu anayekuchukia amelemewa na mzigo na kuanguka, usimpuuze na kwenda zako. Unapaswa kumsaidia kufungua mnyama huyo.+
6 “Usipotoshe uamuzi wa kesi ya maskini aliye miongoni mwenu.+
7 “Jiepushe kabisa na shtaka* la uwongo, na usimuue mtu asiye na hatia na pia mwadilifu, kwa maana sitamtangaza mwovu kuwa mwadilifu.*+
8 “Hupaswi kukubali rushwa, kwa maana rushwa huwapofusha watu wanaoona vizuri na inaweza kupotosha maneno ya watu wenye haki.+
9 “Hupaswi kumkandamiza mkaaji mgeni. Mnajua jinsi mgeni anavyohisi,* kwa sababu mlikuwa wakaaji wageni katika nchi ya Misri.+
10 “Kwa miaka sita utapanda mbegu katika shamba lako na kuvuna mazao yake.+ 11 Lakini mwaka wa saba hutalilima, utaliacha lipumzike, nao maskini walio miongoni mwa watu wako watapata chakula humo, na watakachoacha kitaliwa na wanyama wa mwituni. Hivyo ndivyo utakavyolifanyia shamba lako la mizabibu na shamba lako la mizeituni.
12 “Kwa siku sita utafanya kazi zako; lakini siku ya saba hutafanya kazi, ili ng’ombe dume wako na punda wako wapumzike na mwana wa kijakazi wako na mkaaji mgeni waweze kujiburudisha.+
13 “Unapaswa kuwa mwangalifu kufanya mambo yote niliyokuambia,+ nawe hupaswi kutaja majina ya miungu mingine; yasisikike midomoni*+ mwako.
14 “Unapaswa kunifanyia sherehe mara tatu kwa mwaka.+ 15 Utaadhimisha Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu.+ Utakula mikate isiyo na chachu kwa siku saba, kama nilivyokuamuru, wakati uliowekwa katika mwezi wa Abibu,*+ kwa sababu ulitoka Misri wakati huo. Mtu yeyote asije mbele zangu mikono mitupu.+ 16 Pia, unapaswa kuadhimisha Sherehe ya Mavuno* ya matunda ya kwanza yaliyoiva* ya kazi zako, na ya vitu unavyopanda shambani;+ na Sherehe ya Kukusanya* mwishoni mwa mwaka, unapokusanya mazao ya kazi zako.+ 17 Mara tatu kwa mwaka wanaume wako wote wanapaswa kuja mbele za Bwana wa kweli, Yehova.+
18 “Hupaswi kutoa damu ya dhabihu yangu pamoja na kitu chochote kilichotiwa chachu. Na dhabihu za mafuta zinazotolewa katika sherehe zangu hazipaswi kukaa usiku kucha mpaka asubuhi.
19 “Unapaswa kuleta katika nyumba yangu mimi, Yehova Mungu wako, mazao bora ya kwanza yaliyokomaa* ya ardhi yako.+
“Usimchemshe mwanambuzi katika maziwa ya mama yake.+
20 “Ninamtuma malaika awatangulie+ ili awalinde safarini na kuwapeleka mahali nilipotayarisha.+ 21 Msikilizeni, na mtii sauti yake. Msimwasi, kwa maana hatawasamehe maasi yenu,+ kwa sababu jina langu limo ndani yake. 22 Hata hivyo, mkiitii kabisa sauti yake na kufanya yote ninayowaambia, nitakuwa adui wa maadui wenu na kuwapinga wale wanaowapinga. 23 Kwa maana malaika wangu atawatangulia na kuwapeleka katika nchi ya Waamori, Wahiti, Waperizi, Wakanaani, Wahivi, na Wayebusi, nami nitawaangamiza.+ 24 Hampaswi kuiinamia miungu yao wala kushawishiwa kuiabudu, nanyi hampaswi kuiga mazoea yao.+ Badala yake, mnapaswa kuharibu kabisa sanamu zao na kuvunjavunja nguzo zao takatifu.+ 25 Mnapaswa kunitumikia mimi, Yehova Mungu wenu,+ nami nitabariki mkate wenu na maji yenu.+ Nitaondoa magonjwa miongoni mwenu.+ 26 Hakuna mwanamke katika nchi yenu ambaye mimba yake itaharibika wala atakayekuwa tasa,+ nami nitawapa maisha marefu.*
27 “Nitafanya watu waniogope hata kabla hamjafika,+ nami nitawavuruga watu wote mtakaokutana nao, nami nitawafanya maadui wenu wote washindwe na kukimbia.*+ 28 Nitawafanya Wahivi, Wakanaani, na Wahiti wavunjike moyo* kabla hamjafika,+ nao watawakimbia.+ 29 Sitawafukuza watoke mbele yenu kwa mwaka mmoja, ili nchi isibaki ukiwa na wanyama wa mwituni waongezeke na kuwashambulia.+ 30 Nitawafukuza hatua kwa hatua kutoka mbele yenu, mpaka mtakapoongezeka na kuwa wengi na kuimiliki nchi hiyo.+
31 “Nitaweka mpaka wenu kuanzia Bahari Nyekundu mpaka bahari ya Wafilisti na kuanzia nyikani mpaka kwenye Mto Efrati;+ kwa maana nitawatia wakaaji wa nchi hiyo mikononi mwenu, nanyi mtawafukuza kutoka mbele yenu.+ 32 Hampaswi kufanya agano pamoja nao wala na miungu yao.+ 33 Hawapaswi kuishi katika nchi yenu, wasije wakasababisha mnitendee dhambi. Mkiiabudu miungu yao, kwa hakika itakuwa mtego kwenu.”+
24 Kisha akamwambia Musa: “Panda uje kwangu mimi Yehova, wewe na Haruni, Nadabu na Abihu,+ na wazee 70 wa Israeli, nanyi mwiname chini mkiwa mbali. 2 Musa anapaswa kunikaribia mimi, Yehova, akiwa peke yake; lakini wale wengine hawapaswi kunikaribia, na watu hawapaswi kupanda pamoja naye.”+
3 Kisha Musa akaja na kuwaambia watu maneno yote ya Yehova na sheria zote,*+ na watu wote wakajibu hivi kwa sauti moja: “Maneno yote ambayo Yehova amesema, tuko tayari kuyafanya.”+ 4 Basi Musa akaandika maneno yote ya Yehova.+ Kisha akaamka asubuhi na mapema na kujenga madhabahu kwenye sehemu ya chini ya mlima huo na nguzo 12 kulingana na idadi ya makabila 12 ya Israeli. 5 Baada ya hayo akawatuma wanaume vijana Waisraeli, nao wakatoa dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ng’ombe dume ili ziwe dhabihu za ushirika+ kwa Yehova. 6 Kisha Musa akachukua nusu ya damu ya wanyama hao na kuitia ndani ya mabakuli, na nusu ya damu hiyo akainyunyiza kwenye madhabahu. 7 Halafu akachukua kitabu cha agano na kuwasomea watu kwa sauti.+ Nao wakasema: “Mambo yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya, nasi tutatii.”+ 8 Basi Musa akachukua damu akawanyunyizia watu+ na kusema: “Hii ndiyo damu ya agano ambalo Yehova amefanya pamoja nanyi kulingana na maneno hayo yote.”+
9 Musa na Haruni, Nadabu na Abihu, na wazee 70 wa Israeli wakapanda mlimani, 10 nao wakamwona Mungu wa Israeli.+ Chini ya miguu yake palikuwa na kitu kilichoonekana kama sakafu ya yakuti, nacho kilikuwa safi kama mbingu zenyewe.+ 11 Hakuwadhuru wanaume hao wenye kuheshimika wa Israeli,+ nao walipata maono ya Mungu wa kweli, wakala na kunywa.
12 Sasa Yehova akamwambia Musa: “Panda uje kwangu mlimani na ukae huku. Nitakupa mabamba ya mawe yenye sheria na amri nitakazoandika ili kuwafundisha watu.”+ 13 Basi Musa akaondoka pamoja na Yoshua mhudumu wake,+ naye Musa akapanda kwenye mlima wa Mungu wa kweli.+ 14 Lakini alikuwa amewaambia wale wazee: “Tungojeeni hapa mpaka tutakaporudi.+ Haruni na Huru+ wako pamoja nanyi. Yeyote aliye na kesi anaweza kuwapelekea.”+ 15 Ndipo Musa akapanda mlimani wingu lilipokuwa likiufunika mlima huo.+
16 Utukufu wa Yehova+ uliendelea kukaa juu ya Mlima Sinai,+ na wingu likaufunika kwa siku sita. Siku ya saba akamwita Musa kutoka katikati ya lile wingu. 17 Kwa Waisraeli waliokuwa wakitazama, utukufu wa Yehova ulionekana kama moto mkali kwenye kilele cha mlima. 18 Ndipo Musa akaingia ndani ya lile wingu na kupanda mlimani.+ Musa akakaa mlimani siku 40, mchana na usiku.+
25 Kisha Yehova akamwambia Musa: 2 “Waambie Waisraeli wanitolee mchango; mnapaswa kuchukua mchango wangu kutoka kwa kila mtu ambaye moyo wake unamchochea kuchanga.+ 3 Huu ndio mchango utakaopokea kutoka kwao: dhahabu,+ fedha,+ shaba,+ 4 nyuzi za bluu, sufu ya zambarau,* kitambaa cha rangi nyekundu,* kitani bora, manyoya ya mbuzi, 5 ngozi za kondoo dume zilizotiwa rangi nyekundu, ngozi za sili,* mbao za mshita,+ 6 mafuta kwa ajili ya taa,+ mafuta ya zeri ya kutengenezea mafuta yanayotumiwa kutia mafuta+ na kwa ajili ya uvumba uliotiwa manukato,+ 7 na mawe ya shohamu na mawe mengine ya kupambia efodi+ na kifuko cha kifuani.+ 8 Mtanijengea mahali patakatifu, nami nitakaa* miongoni mwenu.+ 9 Mtatengeneza mahali hapo patakatifu, yaani, hema la ibada pamoja na vyombo vyake vyote, mkifuata kikamili kielelezo nitakachowaonyesha.*+
10 “Mtanitengenezea sanduku la mbao za mshita lenye urefu wa mikono miwili na nusu* na upana wa mkono mmoja na nusu na kimo cha mkono mmoja na nusu.+ 11 Kisha utalifunika kwa dhahabu safi.+ Utalifunika ndani na nje na kutengeneza ukingo wa dhahabu kulizunguka.+ 12 Nawe utatengeneza pete nne za dhahabu na kuzifunga sehemu ya juu ya miguu yake minne, pete mbili upande mmoja na pete mbili upande wa pili. 13 Nawe utatengeneza fito za mshita na kuzifunika kwa dhahabu.+ 14 Utazitia fito hizo katika zile pete zilizo kwenye pande mbili za Sanduku ili zitumiwe kulibeba. 15 Fito hizo zitakaa kwenye pete za Sanduku; hazipaswi kuondolewa.+ 16 Nawe utaweka ndani ya sanduku hilo mabamba ya ushahidi nitakayokupa.+
17 “Utatengeneza kifuniko cha dhahabu safi chenye urefu wa mikono miwili na nusu na upana wa mkono mmoja na nusu.+ 18 Nawe utatengeneza makerubi wawili wa dhahabu; utawatengeneza kwa nyundo kwenye miisho miwili ya kifuniko hicho.+ 19 Tengeneza kerubi mmoja kwenye mwisho mmoja na kerubi mwingine kwenye mwisho wa pili wa kifuniko. 20 Makerubi hao watakuwa wamenyoosha mabawa yao mawili kuelekea juu, na hivyo kukifunika kifuniko hicho kwa mabawa yao,+ nao wataelekeana. Nyuso za makerubi hao zitatazama kifuniko. 21 Utakiweka kifuniko+ hicho juu ya Sanduku, na ndani ya Sanduku utaweka mabamba ya ushahidi nitakayokupa. 22 Nitakutokea hapo na kuzungumza nawe kutoka juu ya kifuniko hicho.+ Kutoka katikati ya hao makerubi wawili walio juu ya sanduku la Ushahidi, nitakujulisha amri zote utakazowapa Waisraeli.
23 “Pia utatengeneza meza+ ya mbao za mshita yenye urefu wa mikono miwili na upana wa mkono mmoja na kimo cha mkono mmoja na nusu.+ 24 Utaifunika kwa dhahabu safi na kutengeneza ukingo wa dhahabu kuizunguka. 25 Utatengeneza utepe wenye upana wa kiganja kimoja* kuizunguka na ukingo wa dhahabu kuzunguka utepe huo. 26 Utaitengenezea pete nne za dhahabu na kuzitia kwenye pembe nne za miguu yake minne, sehemu ambazo miguu hiyo minne inaungana na meza. 27 Pete hizo zitakuwa karibu na utepe ili zitiwe fito za kubebea meza hiyo. 28 Utatengeneza fito za mshita na kuzifunika kwa dhahabu, nanyi mtazitumia kubebea meza hiyo.
29 “Pia utatengeneza sahani, vikombe, magudulia, na mabakuli ya meza hiyo, vitu ambavyo watatumia kumimina matoleo ya vinywaji. Utatengeneza vyombo hivyo kwa dhahabu safi.+ 30 Nawe utaweka mikate ya wonyesho juu ya meza hiyo ili iwe mbele zangu daima.+
31 “Utatengeneza kinara cha taa+ cha dhahabu safi. Kinara hicho cha taa kitatengenezwa kwa nyundo. Sehemu yake ya chini, shina lake, matawi yake, vikombe vyake, matumba yake, na maua yake yatatengenezwa kwa kipande kimoja cha dhahabu.+ 32 Kinara hicho kitakuwa na matawi sita, matawi matatu upande mmoja na matawi matatu upande wa pili. 33 Kila tawi litakuwa na vikombe vitatu vyenye umbo la maua ya mlozi; kila kikombe kitakuwa na ua na tumba lake. Hivyo ndivyo matawi hayo sita yatakavyotengenezwa kwenye shina la kinara hicho cha taa. 34 Kwenye shina la kinara hicho utatengeneza vikombe vinne vyenye umbo la maua ya mlozi, kila kikombe kitakuwa na ua na tumba lake. 35 Kutakuwa na tumba chini ya jozi ya kwanza ya matawi hayo sita, tumba chini ya jozi ya pili, na tumba chini ya jozi ya tatu. 36 Matumba na matawi yake na kinara chote cha taa kitatengenezwa kwa kipande kimoja cha dhahabu safi, kwa kutumia nyundo.+ 37 Utatengeneza taa saba kwa ajili ya kinara hicho, na taa hizo zinapowashwa zitaangaza mbele ya kinara hicho.+ 38 Koleo zake na vyetezo vyake vitatengenezwa kwa dhahabu safi.+ 39 Kinara hicho, pamoja na vifaa hivyo vinapaswa kutengenezwa kwa talanta moja* ya dhahabu safi. 40 Hakikisha kwamba unatengeneza vitu hivyo kwa kufuata kielelezo* ulichoonyeshwa mlimani.+
26 “Utatengeneza hema la ibada+ kwa vitambaa kumi vya kitani bora kilichosokotwa, pia kwa nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, na kitambaa cha rangi nyekundu. Utavitarizi+ kwa michoro+ ya makerubi. 2 Kila kitambaa cha hema la ibada kitakuwa na urefu wa mikono 28* na upana wa mikono 4. Vitambaa vyote vitakuwa na ukubwa uleule.+ 3 Vitambaa vitano vya hema la ibada vitaunganishwa pamoja na kuwa kitambaa kimoja kirefu, na vitambaa vile vingine vitano vitaunganishwa pamoja na kuwa kitambaa kimoja kirefu. 4 Utatengeneza vitanzi vya nyuzi za bluu kwenye upindo wa kitambaa cha mwisho, nawe utafanya vivyo hivyo kwenye upindo wa kitambaa kile kingine mahali ambapo vitaunganishwa. 5 Utatengeneza vitanzi 50 kwenye kitambaa kimoja na vitanzi vingine 50 kwenye upindo wa kitambaa cha pili ili vitanzi hivyo vielekeane vitakapounganishwa. 6 Nawe utatengeneza vibanio 50 vya dhahabu na kuunganisha vitambaa hivyo pamoja kwa vibanio hivyo, ili hema la ibada liwe na kitambaa kimoja kizima.+
7 “Pia utatengeneza vitambaa vya manyoya ya mbuzi+ vya kufunika hema hilo. Utatengeneza vitambaa 11 vya hema.+ 8 Kila kitambaa kitakuwa na urefu wa mikono 30 na upana wa mikono 4. Vitambaa vyote 11 vitakuwa na ukubwa uleule. 9 Utaunganisha vitambaa vitano pamoja na vitambaa sita pamoja, na kitambaa cha sita utakikunja upande wa mbele wa hema. 10 Kisha utatengeneza vitanzi 50 kwenye upindo wa kitambaa cha kwanza, kwenye kipande cha mwisho kabisa, na vitanzi 50 kwenye upindo wa kitambaa cha pili, mahali vitakapounganishwa. 11 Nawe utatengeneza vibanio 50 vya shaba na kuvitia kwenye vitanzi na kuunganisha vitambaa hivyo pamoja, ili hema liwe na kitambaa kimoja kizima. 12 Sehemu inayobaki ya vitambaa vya hema itaning’inia. Nusu inayobaki ya kitambaa cha hema itaning’inia upande wa nyuma wa hema. 13 Sehemu inayobaki ya vitambaa hivyo itaning’inia pande zote za hema kwa urefu wa mkono mmoja kila upande, ili kulifunika hema.
14 “Utatengeneza pia kifuniko kingine cha hema kwa kutumia ngozi za kondoo dume zilizotiwa rangi nyekundu na juu yake kifuniko cha ngozi za sili.+
15 “Utatengeneza viunzi vya mbao+ za mshita vilivyo wima kwa ajili ya hema hilo.+ 16 Kila kiunzi kitakuwa na urefu wa mikono kumi na upana wa mkono mmoja na nusu. 17 Kila kiunzi kitakuwa na ndimi mbili* zilizounganishwa pamoja. Hivyo ndivyo utakavyotengeneza viunzi vyote vya hema la ibada. 18 Utatengeneza viunzi 20 kwa ajili ya upande wa kusini wa hema la ibada.
19 “Utatengeneza vikalio 40 vya fedha+ chini ya vile viunzi 20: vikalio viwili chini ya kiunzi kimoja pamoja na ndimi zake mbili, na vikalio viwili chini ya kila kiunzi kinachofuata pamoja na ndimi zake mbili.+ 20 Utatengeneza viunzi 20 upande wa pili wa hema, upande wa kaskazini 21 pamoja na vikalio vyake 40 vya fedha, vikalio viwili chini ya kiunzi kimoja na vikalio viwili chini ya kila kiunzi kinachofuata. 22 Utatengeneza viunzi sita sehemu ya nyuma ya hema la ibada, upande wa magharibi.+ 23 Nawe utatengeneza viunzi viwili viwe mihimili miwili ya pembeni upande wa nyuma wa hema la ibada. 24 Katika pembe zote mbili kutakuwa na viunzi viwili kuanzia sehemu ya chini mpaka sehemu ya juu, kwenye pete ya kwanza. Hivyo ndivyo utakavyotengeneza viunzi vyote viwili; vitakuwa mihimili miwili ya pembeni. 25 Kutakuwa na viunzi vinane na vikalio vyake 16 vya fedha, vikalio viwili chini ya kiunzi kimoja na vikalio viwili chini ya kila kiunzi kinachofuata.
26 “Utatengeneza fito za mshita, fito tano kwa ajili viunzi vya upande mmoja wa hema la ibada,+ 27 na fito tano kwa ajili ya viunzi vya upande wa pili wa hema la ibada, na fito tano kwa ajili ya viunzi vya sehemu ya nyuma ya hema la ibada, upande wa magharibi. 28 Ufito ulio katikati ya viunzi utatoka mwisho mmoja mpaka mwingine.
29 “Nawe utavifunika viunzi hivyo kwa dhahabu+ na kutengeneza pete za dhahabu ili zishikilie fito, na fito hizo utazifunika kwa dhahabu. 30 Utatengeneza hema la ibada kwa kufuata ramani ambayo nilikupa mlimani.+
31 “Utatengeneza pazia+ la nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa. Utalitarizi kwa michoro ya makerubi. 32 Utalining’iniza kwenye nguzo nne za mshita zilizofunikwa kwa dhahabu. Kulabu zake zitakuwa za dhahabu. Nguzo hizo zitakaa juu ya vikalio vinne vya fedha. 33 Utalining’iniza pazia hilo chini ya vibanio na kuleta sanduku la Ushahidi+ humo, nyuma ya pazia. Pazia hilo litatenganisha Patakatifu+ na Patakatifu Zaidi.+ 34 Utaweka kile kifuniko juu ya sanduku la Ushahidi ndani ya Patakatifu Zaidi.
35 “Utaiweka ile meza nje ya pazia, na kinara cha taa+ kitaelekeana na meza hiyo upande wa kusini wa hema la ibada; utaiweka meza upande wa kaskazini. 36 Kwa ajili ya mlango wa hema, utatengeneza pazia la nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa na kufumwa.+ 37 Utatengeneza nguzo tano za mshita na kuzifunika kwa dhahabu kwa ajili ya pazia hilo. Kulabu zake zitakuwa za dhahabu, nawe utazitengenezea vikalio vitano vya shaba.
27 “Utatengeneza madhabahu kwa mbao za mshita;+ itakuwa na urefu wa mikono mitano* na upana wa mikono mitano. Madhabahu hiyo itakuwa ya mraba na kimo chake kitakuwa mikono mitatu.+ 2 Utatengeneza pembe+ kwenye ncha zake nne; pembe hizo zitakuwa sehemu ya madhabahu, nawe utaifunika madhabahu hiyo kwa shaba.+ 3 Utatengeneza ndoo za kuondolea majivu,* pia sepetu, mabakuli, nyuma,* na vyetezo; utatengeneza vyombo vyote vya madhabahu kwa shaba.+ 4 Nawe utatengeneza wavu wa shaba kwa ajili ya madhabahu, pia utatengeneza pete nne za shaba kwenye pembe nne za wavu huo. 5 Nawe utauweka wavu huo chini ya ukingo wa madhabahu, nao utashuka ndani ya madhabahu kufikia katikati. 6 Utatengeneza fito za mshita kwa ajili ya madhabahu na kuzifunika kwa shaba. 7 Fito hizo zitaingizwa kwenye zile pete ili ziwe katika pande mbili za madhabahu wakati inapobebwa.+ 8 Utaitengeneza madhabahu hiyo kama sanduku la mbao lenye uwazi. Inapaswa kutengenezwa kama tu Alivyokuonyesha mlimani.+
9 “Utatengeneza ua wa hema+ la ibada. Upande wa kusini, ua huo utakuwa na mapazia yanayoning’inia ya kitani bora kilichosokotwa; yatakuwa na urefu wa mikono 100 upande mmoja.+ 10 Ua huo utakuwa na nguzo 20 na vikalio 20 vya shaba. Kulabu za nguzo hizo pamoja na vitanzi* vyake vitakuwa vya fedha. 11 Mapazia yanayoning’inia upande wa kaskazini yatakuwa pia na urefu wa mikono 100, pamoja na nguzo zake 20 na vikalio vyake 20 vya shaba, lakini kulabu za nguzo hizo na vitanzi* vyake vitakuwa vya fedha. 12 Upande wa magharibi wa ua utakuwa na mapazia yanayoning’inia yenye urefu wa mikono 50, na nguzo 10 na vikalio 10. 13 Ua utakuwa na upana wa mikono 50 upande wa mashariki, yaani, upande wa mapambazuko ya jua. 14 Mapazia yanayoning’inia yenye upana wa mikono 15 yatakuwa upande mmoja, pamoja na nguzo tatu na vikalio vitatu.+ 15 Upande wa pili utakuwa na mapazia yanayoning’inia yenye upana wa mikono 15, pamoja na nguzo tatu na vikalio vitatu.
16 “Mlango wa ua utakuwa na pazia lenye urefu wa mikono 20 lililotengenezwa kwa nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa na kufumwa,+ pamoja na nguzo nne na vikalio vyake vinne.+ 17 Nguzo zote zinazozunguka ua zitakuwa na kulabu na vitanzi vya fedha, lakini vikalio vyake vitakuwa vya shaba.+ 18 Ua huo utakuwa na urefu wa mikono 100,+ upana wa mikono 50, na kimo cha mikono 5, nao utatengenezwa kwa kitani bora kilichosokotwa, na utakuwa na vikalio vya shaba. 19 Vyombo na vitu vyote vitakavyotumiwa katika utumishi wa hema la ibada, pamoja na vigingi vyote vya hema na vya ua, vitakuwa vya shaba.+
20 “Utawaamuru Waisraeli wakuletee mafuta safi ya zeituni zilizopondwa ili taa ziwake daima.+ 21 Katika hema la mkutano, nje ya pazia lililo karibu na sanduku la Ushahidi,+ Haruni na wanawe watahakikisha kwamba taa hizo zinawaka kuanzia jioni mpaka asubuhi mbele za Yehova.+ Hiyo ni sheria ya kudumu katika vizazi vyao vyote itakayotekelezwa na Waisraeli.+
28 “Utamleta Haruni+ ndugu yako pamoja na wanawe,+ Nadabu na Abihu,+ Eleazari na Ithamari+ kutoka miongoni mwa Waisraeli ili wanitumikie+ wakiwa makuhani. 2 Utamtengenezea Haruni ndugu yako mavazi matakatifu ili awe na utukufu na fahari.+ 3 Waambie mafundi wote wenye ustadi,* ambao nimewajaza roho ya hekima,+ wamtengenezee Haruni mavazi ili kumtakasa, ili anitumikie akiwa kuhani.
4 “Haya ndiyo mavazi watakayotengeneza: kifuko cha kifuani,+ efodi,+ joho lisilo na mikono,+ kanzu yenye miraba, kilemba,+ na ukumbuu;+ watamtengenezea Haruni na wanawe mavazi haya matakatifu ili wanitumikie wakiwa makuhani. 5 Mafundi hao stadi watatumia dhahabu, nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora.
6 “Watatengeneza efodi kwa dhahabu, nyuzi za bluu, sufu ya rangi ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa, nacho kinapaswa kutariziwa.+ 7 Efodi itakuwa na vipande viwili vitakavyounganishwa kwenye miisho miwili mabegani. 8 Mshipi uliofumwa+ unaoshikilia kwa nguvu efodi unapaswa kutengenezwa kwa vitu hivyohivyo, yaani, dhahabu, nyuzi za bluu, sufu ya rangi ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa.
9 “Utachukua mawe mawili ya shohamu+ na kuchonga juu yake majina ya wana wa Israeli,+ 10 majina sita juu ya jiwe moja na majina mengine sita juu ya jiwe lingine, kulingana na umri wao. 11 Mchonga mawe atachonga majina ya wana wa Israeli kwenye mawe hayo mawili kama mtu anavyochonga muhuri.+ Kisha mawe hayo yatatiwa katika vifuko vya dhahabu. 12 Utayaweka mawe hayo mawili kwenye vipande vya mabegani vya efodi, nayo yatakuwa mawe ya ukumbusho kwa wana wa Israeli,+ naye Haruni atayabeba majina yao kwenye vipande viwili vya efodi mabegani mwake kama ukumbusho mbele za Yehova. 13 Utatengeneza vifuko vya dhahabu 14 na minyororo miwili ya dhahabu safi iliyosokotwa kama kamba,+ utaifunga minyororo hiyo kwenye vifuko hivyo.+
15 “Utamwagiza fundi wa kutarizi atengeneze kifuko cha kifuani cha maamuzi.+ Atakitengeneza kama efodi, kwa kutumia dhahabu, nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa.+ 16 Kifuko hicho kinapaswa kuwa cha mraba kinapokunjwa mara mbili, urefu wake uwe shubiri moja* na upana wake shubiri moja. 17 Unapaswa kuweka kwenye kifuko hicho mawe yaliyopangwa katika safu nne. Safu ya kwanza itakuwa na zabarijadi, topazi, na zumaridi. 18 Safu ya pili itakuwa na feruzi, yakuti, na yaspi. 19 Safu ya tatu itakuwa na jiwe la leshemi,* akiki, na amethisti. 20 Safu ya nne itakuwa na krisolito, shohamu, na yashefi. Mawe hayo yatawekwa kwenye vifuko vya dhahabu. 21 Mawe hayo yatalingana na majina 12 ya wana wa Israeli. Kila jina linapaswa kuchongwa kama muhuri unavyochongwa, na kila jina litawakilisha mojawapo ya makabila 12 ya wana wa Israeli.
22 “Utakitengenezea kifuko cha kifuani minyororo iliyosokotwa, kama kamba za dhahabu safi.+ 23 Pia utakitengenezea pete mbili za dhahabu na kuzitia kwenye pembe mbili za juu za kifuko hicho. 24 Utatia zile kamba mbili za dhahabu katika pete mbili zilizo kwenye pembe za kifuko cha kifuani. 25 Kisha utatia ncha mbili za zile kamba mbili katika vile vifuko viwili vya mabegani, nawe unapaswa kuzifunga ncha hizo kwenye vipande viwili vya efodi, sehemu ya mbele. 26 Utatengeneza pete mbili za dhahabu na kuziweka kwenye pembe mbili za chini, upande wa ndani wa kifuko cha kifuani, upande wa efodi.+ 27 Utatengeneza pete nyingine mbili za dhahabu upande wa mbele wa efodi, chini ya vipande viwili vya mabegani vya efodi, karibu na mahali inapoungana, juu ya mshipi uliofumwa wa efodi.+ 28 Pete za kifuko cha kifuani zitafungwa pamoja na pete za efodi kwa kamba ya bluu. Hivyo, kifuko cha kifuani kitabaki mahali pake kwenye efodi, juu ya mshipi uliofumwa.
29 “Haruni atayabeba majina ya wana wa Israeli juu ya moyo wake kwenye kile kifuko cha kifuani cha maamuzi anapoingia Patakatifu kama ukumbusho wa daima mbele za Yehova. 30 Utaweka Urimu na Thumimu*+ ndani ya kifuko cha kifuani cha maamuzi, nazo zitakuwa juu ya moyo wa Haruni anapoingia mbele za Yehova, naye Haruni atabeba daima juu ya moyo wake vitu hivyo vya kufanyia maamuzi kwa ajili ya Waisraeli mbele za Yehova.
31 “Utatengeneza joho lisilo na mikono la efodi kwa nyuzi za bluu peke yake.+ 32 Litakuwa na nafasi ya kupitishia kichwa katikati upande wa juu. Sehemu hiyo itakuwa na ukingo uliofumwa kuizunguka. Itakuwa na ukingo kama wa koti la vita ili isiraruke. 33 Kwenye upindo wake wote, utatengeneza makomamanga ya nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kutia kengele za dhahabu katikati ya makomamanga. 34 Utatia kengele ya dhahabu kisha komamanga, kengele ya dhahabu kisha komamanga, kwenye upindo wote wa joho hilo lisilo na mikono. 35 Ni lazima Haruni alivae anapohudumu, na sauti ya kengele hizo inapaswa kusikika anapoingia patakatifu mbele za Yehova na anapotoka nje, ili asife.+
36 “Utatengeneza bamba linalong’aa la dhahabu safi na kuchonga maneno haya juu yake kama muhuri unavyochongwa: ‘Utakatifu ni wa Yehova.’+ 37 Ni lazima ulifunge bamba hilo kwenye kilemba+ kwa kamba ya bluu; litakuwa daima upande wa mbele wa kilemba. 38 Nalo litakuwa kwenye paji la uso wa Haruni, naye Haruni atawajibika Mwisraeli anapotenda kosa dhidi ya vitu vitakatifu+ vinavyotakaswa na Waisraeli wakati wanapovitoa kuwa zawadi takatifu. Ni lazima bamba hilo likae sikuzote kwenye paji la uso wake, ili wapate kibali mbele za Yehova.
39 “Utafuma kanzu ya kitani bora yenye miraba, utatengeneza kilemba cha kitani bora, na kufuma ukumbuu.+
40 “Pia utawatengenezea wana wa Haruni kanzu,+ ukumbuu, na kofia, ili wawe na utukufu na fahari.+ 41 Utamvisha Haruni ndugu yako na wanawe mavazi hayo, nawe utawatia mafuta+ na kuwaweka rasmi*+ na kuwatakasa, nao watanitumikia wakiwa makuhani. 42 Pia watengenezee suruali fupi* za kitani ili kufunika uchi wao.+ Suruali hizo zitawafunika kuanzia kiunoni mpaka mapajani. 43 Haruni na wanawe watazivaa wanapoingia kwenye hema la mkutano au wanapokaribia madhabahu kuhudumu mahali patakatifu, ili wasipatwe na hatia na kufa. Ni sheria ya kudumu kwa Haruni na uzao wake.*
29 “Hivi ndivyo utakavyowatakasa ili wanitumikie wakiwa makuhani: Chukua ng’ombe dume mchanga, kondoo dume wawili wasio na kasoro,+ 2 mikate isiyo na chachu, mikate ya mviringo isiyo na chachu na iliyokandwa kwa mafuta, na mikate myembamba isiyo na chachu na ambayo imepakwa mafuta.+ Utaioka kwa unga laini wa ngano 3 na kuiweka ndani ya kikapu, nawe utaileta mbele zangu ikiwa ndani ya kikapu,+ pamoja na yule ng’ombe dume na wale kondoo dume wawili.
4 “Utamleta Haruni na wanawe kwenye mlango wa hema la mkutano+ na kuwaosha kwa maji.+ 5 Kisha utachukua yale mavazi+ na kumvisha Haruni kanzu, joho la efodi lisilo na mikono, efodi, na kifuko cha kifuani, nawe utamfunga vizuri kabisa kiunoni ule mshipi uliofumwa wa efodi.+ 6 Utamvisha kile kilemba kichwani na kuiweka ile ishara takatifu ya wakfu* kwenye kilemba hicho;+ 7 kisha chukua mafuta yanayotumiwa kutia mafuta+ na uyamimine juu ya kichwa chake na kumtia mafuta.+
8 “Halafu walete wanawe na kuwavisha kanzu+ 9 na umfunge Haruni na wanawe ukumbuu viunoni na kuwavisha kofia zao; ukuhani utakuwa wao, nayo itakuwa sheria ya kudumu.+ Hivyo ndivyo utakavyowaweka rasmi Haruni na wanawe ili watumike wakiwa makuhani.*+
10 “Sasa utamleta yule ng’ombe dume mbele ya hema la mkutano, na Haruni na wanawe wataweka mikono yao juu ya kichwa cha huyo ng’ombe dume.+ 11 Mchinje huyo ng’ombe dume mbele za Yehova, kwenye mlango wa hema la mkutano.+ 12 Chukua kiasi fulani cha damu ya huyo ng’ombe dume kwa kidole chako na kuitia kwenye pembe za madhabahu,+ kisha umwage damu yote inayobaki chini kwenye msingi wa madhabahu.+ 13 Kisha chukua mafuta yote+ yanayofunika matumbo, mafuta yaliyo juu ya ini, na figo zake mbili na mafuta yaliyo juu yake, nawe uchome moto vitu hivyo ili vifuke moshi juu ya madhabahu.+ 14 Lakini nyama ya ng’ombe dume huyo na ngozi yake na mavi yake utaviteketeza nje ya kambi. Hiyo ni dhabihu ya dhambi.
15 “Kisha utamchukua kondoo dume mmoja, naye Haruni na wanawe wataweka mikono yao juu ya kichwa cha huyo kondoo dume.+ 16 Mchinje kondoo dume huyo, uchukue damu yake na kuinyunyiza pande zote za madhabahu.+ 17 Mkate kondoo dume huyo vipandevipande, uoshe matumbo yake+ na miguu yake, na kuvipanga vipande hivyo pamoja na kichwa chake. 18 Utamchoma moto huyo kondoo mzima ili afuke moshi juu ya madhabahu. Ni dhabihu ya kuteketezwa kwa Yehova, harufu inayompendeza.*+ Ni dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto.
19 “Kisha utamchukua kondoo dume wa pili, na Haruni na wanawe wataweka mikono yao juu ya kichwa cha kondoo huyo.+ 20 Mchinje kondoo dume huyo na uchukue kiasi fulani cha damu yake na kuipaka kwenye ncha ya sikio la kulia la Haruni na kwenye ncha za masikio ya kulia ya wanawe na kwenye vidole gumba vya mikono yao ya kulia na kwenye vidole gumba vya miguu yao ya kulia, nawe unyunyize damu pande zote za madhabahu. 21 Kisha chukua kiasi fulani cha damu iliyo kwenye madhabahu na baadhi ya mafuta yanayotumiwa kutia mafuta,+ nawe umnyunyizie Haruni na mavazi yake na wanawe na mavazi yao, ili awe mtakatifu yeye na mavazi yake na wanawe na mavazi yao.+
22 “Halafu chukua mafuta ya huyo kondoo dume, mkia wake mnono, mafuta yanayofunika matumbo, mafuta yaliyo juu ya ini, figo zake mbili na mafuta yaliyo juu yake,+ na mguu wa kulia, kwa maana huyo ni kondoo dume wa kumweka rasmi kuhani.+ 23 Chukua pia mkate wa mviringo na mkate wa mviringo uliokandwa kwa mafuta na mkate mwembamba kutoka katika kile kikapu cha mikate isiyo na chachu kilicho mbele za Yehova. 24 Ni lazima uviweke vitu hivyo vyote mikononi mwa Haruni na mikononi mwa wanawe, nawe utavitikisa kwenda mbele na nyuma vikiwa toleo la kutikiswa mbele za Yehova. 25 Kisha utavichukua vitu hivyo kutoka mikononi mwao na kuviteketeza juu ya madhabahu, juu ya dhabihu ya kuteketezwa, ili viwe harufu inayompendeza* Yehova. Ni dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto.
26 “Halafu chukua kidari cha kondoo dume wa kumweka rasmi kuhani,+ anayetolewa kwa ajili ya Haruni, nawe ukitikise kwenda mbele na nyuma kikiwa toleo la kutikiswa mbele za Yehova, nacho kitakuwa fungu lako. 27 Utakitakasa kidari cha toleo la kutikiswa na ule mguu wa fungu takatifu ambao ulitikiswa na ambao ulichukuliwa kutoka kwa yule kondoo dume wa kumweka rasmi kuhani,+ aliyetolewa kwa ajili ya Haruni na wanawe. 28 Vitu hivyo vitakuwa vya Haruni na wanawe kulingana na sheria ya kudumu itakayotekelezwa na Waisraeli, kwa sababu vitu hivyo ni fungu takatifu, navyo vitakuwa fungu takatifu litakalotolewa na Waisraeli.+ Ni fungu lao takatifu kwa Yehova kutoka katika dhabihu zao za ushirika.+
29 “Mavazi matakatifu+ ya Haruni yatatumiwa na wanawe+ baada yake watakapotiwa mafuta na kuwekwa rasmi kuwa makuhani. 30 Mwana wa Haruni atakayewekwa kuwa kuhani baada yake na ambaye ataingia katika hema la mkutano ili kuhudumu mahali patakatifu atayavaa mavazi hayo kwa siku saba.+
31 “Utamchukua yule kondoo dume wa kumweka rasmi kuhani na kuichemshia nyama yake mahali patakatifu.+ 32 Haruni na wanawe wataila+ nyama ya kondoo dume huyo na mikate iliyo katika kikapu kwenye mlango wa hema la mkutano. 33 Watakula vitu vilivyotolewa dhabihu ili kufunika dhambi wakati walipowekwa rasmi kuwa makuhani* na kutakaswa. Lakini mtu ambaye hana idhini* hapaswi kuvila, kwa maana ni vitakatifu.+ 34 Ikiwa nyama yoyote ya dhabihu ya kumweka rasmi kuhani na mkate wowote utabaki mpaka asubuhi, unapaswa kuteketeza kinachobaki.+ Hakipaswi kuliwa kwa sababu ni kitakatifu.
35 “Hivi ndivyo utakavyomfanyia Haruni na wanawe, kulingana na yote niliyokuamuru. Utatumia siku saba kuwaweka rasmi kuwa makuhani.*+ 36 Kila siku utamtoa ng’ombe dume wa dhabihu ya dhambi ili kufunika dhambi zao, nawe utaitakasa madhabahu kwa kutoa dhabihu ya kufunika dhambi ya madhabahu hiyo, nawe utaitia mafuta ili kuitakasa.+ 37 Utatumia siku saba kufunika dhambi ya madhabahu, nawe lazima uitakase ili iwe madhabahu takatifu kabisa.+ Mtu yeyote anayeigusa madhabahu hiyo anapaswa kuwa mtakatifu.
38 “Hivi ndivyo vitu utakavyotoa kwenye madhabahu: kila siku, kwa kuendelea,+ utatoa wanakondoo dume wawili wenye umri wa mwaka mmoja. 39 Mtoe mwanakondoo dume mmoja asubuhi na yule mwingine jioni kabla ya giza kuingia.*+ 40 Sehemu ya kumi ya kipimo cha efa moja* ya unga laini uliochanganywa na robo ya hini* ya mafuta ya zeituni zilizopondwa, na toleo la kinywaji la robo ya hini ya divai, vitatolewa pamoja na mwanakondoo dume wa kwanza. 41 Utamtoa mwanakondoo dume wa pili jioni kabla ya giza kuingia,* pamoja na matoleo ya nafaka na kinywaji kama yale ya asubuhi. Utamtoa akiwa harufu inayopendeza,* dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto. 42 Itakuwa dhabihu ya kuteketezwa itakayotolewa kwa ukawaida katika vizazi vyenu vyote kwenye mlango wa hema la mkutano mbele za Yehova, mahali ambapo nitawatokea ili kuzungumza nanyi.+
43 “Hapo ndipo nitakapowatokea Waisraeli, na utukufu wangu utapatakasa mahali hapo.+ 44 Nitalitakasa hema la mkutano na madhabahu, nami nitamtakasa Haruni na wanawe+ ili wanitumikie wakiwa makuhani. 45 Nitakaa* miongoni mwa Waisraeli, nami nitakuwa Mungu wao.+ 46 Nao hakika watajua kwamba mimi ni Yehova Mungu wao, niliyewatoa katika nchi ya Misri ili nikae miongoni mwao.+ Mimi ni Yehova Mungu wao.
30 “Utajenga madhabahu ya kufukizia uvumba;+ utaijenga kwa mbao za mshita.+ 2 Itakuwa ya mraba; urefu wa mkono mmoja,* upana wa mkono mmoja, na kimo cha mikono miwili. Pembe zake zitakuwa sehemu ya madhabahu hiyo.+ 3 Utaifunika kwa dhahabu safi: sehemu yake ya juu, pande zote kuizunguka, na pembe zake; nawe utatengeneza ukingo wa dhahabu kuizunguka. 4 Pia, utaitengenezea pete mbili za dhahabu chini ya ukingo wake kwenye pande zake mbili zinazoelekeana, na pete hizo zitashikilia fito za kubebea madhabahu. 5 Tengeneza fito za mshita na kuzifunika kwa dhahabu. 6 Utaiweka mbele ya pazia lililo karibu na sanduku la Ushahidi,+ mbele ya kifuniko kilicho juu ya sanduku la Ushahidi, mahali nitakapokutokea.+
7 “Haruni+ atafukiza uvumba wenye manukato+ juu ya madhabahu hiyo+ kila asubuhi anaposhughulikia taa.+ 8 Pia, Haruni anapowasha taa jioni kabla ya giza kuingia,* atafukiza uvumba. Ni uvumba unaofukizwa kwa ukawaida mbele za Yehova katika vizazi vyenu vyote. 9 Hampaswi kufukiza uvumba usio halali+ au kutoa juu yake dhabihu ya kuteketezwa au toleo la nafaka, wala hampaswi kumimina juu yake toleo la kinywaji. 10 Haruni anapaswa kutoa dhabihu ya kufunika dhambi juu ya pembe za madhabahu hiyo mara moja kwa mwaka.+ Akitumia kiasi fulani cha damu ya dhabihu ya dhambi inayotolewa ili kufunika dhambi,+ ataitakasa mara moja kwa mwaka katika vizazi vyenu vyote. Ni madhabahu takatifu zaidi kwa Yehova.”
11 Kisha Yehova akamwambia Musa: 12 “Wakati wowote unapowahesabu wana wa Israeli,+ ni lazima kila mmoja wao anipe mimi Yehova fidia kwa ajili ya nafsi yake* watu wanapohesabiwa. Watafanya hivyo ili wasipatwe na pigo lolote wanapoandikishwa. 13 Wote watakaoandikishwa watatoa nusu ya shekeli* kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu.*+ Gera 20* ni sawa na shekeli moja. Nusu shekeli ni mchango kwa Yehova.+ 14 Kila mtu mwenye umri wa kuanzia miaka 20 anayeandikishwa atatoa mchango wa Yehova.+ 15 Tajiri hapaswi kutoa zaidi na maskini hapaswi kutoa mchango wa Yehova unaopungua nusu shekeli* ili kutoa dhabihu ya kufunika dhambi kwa ajili ya nafsi zenu.* 16 Unapaswa kuchukua kutoka kwa Waisraeli fedha za dhabihu ya kufunika dhambi na kuzitoa ili zitumiwe katika utumishi wa hema la mkutano, ziwe kumbukumbu mbele za Yehova kwa ajili ya Waisraeli, ili kufunika dhambi kwa ajili ya nafsi zenu.”*
17 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 18 “Tengeneza beseni la kunawia la shaba pamoja na kinara chake;+ kisha uliweke kati ya hema la mkutano na madhabahu na utie maji ndani yake.+ 19 Haruni na wanawe watanawa mikono na miguu yao kwenye beseni hilo.+ 20 Wanapoingia kwenye hema la mkutano au wanapoenda kwenye madhabahu kuhudumu na kumtolea Yehova dhabihu za kuteketezwa na zinazofuka moshi, watanawa kwa maji ili wasife. 21 Ni lazima wanawe mikono na miguu ili wasife, nayo itakuwa sheria ya kudumu kwa ajili yao, yaani, kwa Haruni na uzao wake, katika vizazi vyao vyote.”+
22 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 23 “Kisha, chukua manukato bora kabisa: kilogramu 6 za manemane iliyoganda, kilogramu 3 za mdalasini wenye harufu nzuri, kilogramu 3 za kane, 24 na kilogramu 6 za kida, zilizopimwa kwa shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu,*+ pamoja na hini moja* ya mafuta ya zeituni. 25 Kisha utumie manukato hayo kutengeneza mafuta matakatifu ya kutia mafuta; manukato hayo yanapaswa kuchanganywa pamoja kwa ustadi.*+ Yatakuwa mafuta matakatifu ya kutia mafuta.
26 “Utayatumia kutia mafuta hema la mkutano+ na sanduku la Ushahidi, 27 pamoja na meza na vyombo vyake vyote, kinara cha taa na vyombo vyake, madhabahu ya uvumba, 28 madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa na vyombo vyake vyote, na lile beseni pamoja na kinara chake. 29 Ni lazima uvitakase ili viwe vitakatifu kabisa.+ Yeyote anayevigusa anapaswa kuwa mtakatifu.+ 30 Nawe utamtia mafuta Haruni+ na wanawe+ na kuwatakasa ili wanitumikie wakiwa makuhani.+
31 “Nawe utawaambia Waisraeli, ‘Mafuta haya ya kutia mafuta yataendelea kuwa matakatifu kwangu katika vizazi vyenu.+ 32 Hayapaswi kupakwa kwenye ngozi ya mwanadamu, nanyi hampaswi kutengeneza kitu chochote chenye mchanganyiko kama huo. Ni mafuta matakatifu. Yataendelea kuwa matakatifu kwenu. 33 Mtu yeyote anayetengeneza mafuta kama hayo na kumpaka mtu asiye na idhini* ni lazima auawe.’”+
34 Kisha Yehova akamwambia Musa: “Chukua vipimo vinavyolingana vya manukato haya:+ matone ya natafi, shekelethi, kelbena yenye manukato, na ubani safi. 35 Yatumie kutengeneza uvumba;+ viungo hivyo vinapaswa kuchanganywa kwa ustadi,* vitiwe chumvi,+ viwe safi, na vitakatifu. 36 Utaponda baadhi ya viungo hivyo viwe unga laini na kuweka kiasi fulani mbele ya sanduku la Ushahidi katika hema la mkutano, mahali nitakapokutokea. Mchanganyiko huo unapaswa kuwa mtakatifu kabisa kwenu. 37 Hampaswi kutumia mchanganyiko huo kujitengenezea uvumba kwa ajili ya matumizi yenu.+ Mnapaswa kuuona kuwa mtakatifu kwa Yehova. 38 Yeyote atakayetengeneza uvumba kama huo ili afurahie harufu yake ni lazima auawe.”
31 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Tazama, nimemchagua* Bezaleli+ mwana wa Uri mwana wa Huru wa kabila la Yuda.+ 3 Nitamjaza roho ya Mungu, na kumpa hekima, uelewaji, na ujuzi katika kila aina ya ufundi, 4 ili abuni kazi za usanii akitumia dhahabu, fedha, na shaba, 5 ili achonge na kupamba kwa mawe,+ na kutengeneza vifaa vya mbao vya kila aina.+ 6 Pia, nimemchagua Oholiabu+ mwana wa Ahisamaki wa kabila la Dani ili amsaidie, nami ninaweka hekima katika mioyo ya wote wenye ustadi,* ili watengeneze kila kitu nilichokuamuru:+ 7 hema la mkutano,+ sanduku la Ushahidi+ na kifuniko chake,+ vyombo vyote vya hema, 8 meza+ na vyombo vyake, kinara cha taa cha dhahabu safi na vyombo vyake vyote,+ madhabahu ya uvumba,+ 9 madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa+ na vyombo vyake vyote, beseni na kinara chake,+ 10 yale mavazi bora yaliyofumwa, mavazi matakatifu ya kuhani Haruni, mavazi ya wanawe ya kutumikia wakiwa makuhani,+ 11 mafuta yanayotumiwa kutia mafuta, na ule uvumba wenye manukato kwa ajili ya mahali patakatifu.+ Watafanya mambo yote niliyokuamuru.”
12 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 13 “Waambie Waisraeli, ‘Mnapaswa hasa kushika sabato zangu,+ kwa maana ni ishara kati yangu pamoja nanyi katika vizazi vyenu ili mjue kwamba mimi, Yehova, ninawatakasa ninyi. 14 Ni lazima mshike Sabato kwa sababu ni takatifu kwenu.+ Mtu yeyote atakayeitia unajisi ni lazima auawe. Mtu yeyote atakayefanya kazi siku hiyo, ni lazima auawe kutoka kati ya watu wake.+ 15 Mnaweza kufanya kazi kwa siku sita, lakini siku ya saba ni sabato ya pumziko kamili.+ Ni takatifu kwa Yehova. Mtu yeyote atakayefanya kazi siku ya Sabato ni lazima auawe. 16 Ni lazima Waisraeli washike Sabato; ni lazima waadhimishe Sabato katika vizazi vyao vyote. Ni agano la kudumu. 17 Ni ishara ya kudumu kati yangu na Waisraeli,+ kwa sababu katika siku sita mimi, Yehova, niliziumba mbingu na dunia na katika siku ya saba nilipumzika na kustarehe.’”+
18 Sasa mara tu alipomaliza kuzungumza naye kwenye Mlima Sinai, alimpa Musa mabamba mawili ya Ushahidi,+ mabamba ya mawe yaliyoandikwa kwa kidole cha Mungu.+
32 Basi, watu wakaona kwamba Musa amekawia sana kushuka kutoka mlimani.+ Kwa hiyo wakakusanyika kumzunguka Haruni na kumwambia: “Haya, tutengenezee mungu atakayetuongoza+ kwa sababu hatujui lililompata huyu Musa, mtu aliyetuongoza kutoka katika nchi ya Misri.” 2 Ndipo Haruni akawaambia: “Chukueni vipuli vya dhahabu+ ambavyo wake zenu, wana wenu, na binti zenu wamevaa masikioni mniletee.” 3 Basi watu wote wakaanza kutoa vipuli vya dhahabu walivyokuwa wamevaa masikioni wakamletea Haruni. 4 Kisha akachukua dhahabu iliyokuwa kwenye vipuli hivyo, akatengeneza sanamu* ya ndama kwa kifaa cha kuchongea.+ Watu wakaanza kusema: “Huyu ndiye Mungu wenu, enyi Waisraeli, aliyewaongoza kutoka katika nchi ya Misri.”+
5 Haruni alipoona hilo, akajenga madhabahu mbele ya sanamu hiyo na kutangaza hivi: “Kesho kutakuwa na sherehe kwa ajili ya Yehova.” 6 Basi wakaamka mapema siku iliyofuata na kuanza kutoa dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ushirika. Baada ya hayo watu wakaketi ili wale na kunywa. Kisha wakasimama ili wajitumbuize.+
7 Sasa Yehova akamwambia Musa: “Nenda, shuka, kwa sababu watu wako uliowaongoza kutoka katika nchi ya Misri wametenda uovu.*+ 8 Wamegeuka haraka na kuacha njia niliyowaamuru wafuate.+ Wamejitengenezea sanamu* ya ndama, nao wanaendelea kuiinamia na kuitolea dhabihu wakisema, ‘Huyu ndiye Mungu wenu, enyi Waisraeli, aliyewaongoza kutoka katika nchi ya Misri.’” 9 Yehova akaendelea kumwambia Musa: “Nimeona kwamba watu hawa ni wakaidi.*+ 10 Basi sasa, niache niwaangamize kabisa kwa hasira yangu inayowaka, na acha nikufanye wewe kuwa taifa kubwa.”+
11 Ndipo Musa akamsihi* Yehova Mungu wake+ akisema: “Ee Yehova, kwa nini uwaelekezee watu wako hasira yako inayowaka, baada ya kuwatoa katika nchi ya Misri kwa nguvu kuu na kwa mkono wenye nguvu?+ 12 Kwa nini Wamisri waseme, ‘Alikuwa na nia ovu alipowatoa Misri. Alitaka kuwaua milimani na kuwaangamiza kabisa kutoka duniani’?+ Acha hasira yako inayowaka na ufikirie upya* uamuzi wako wa kuwaletea watu wako msiba huu. 13 Wakumbuke watumishi wako Abrahamu, Isaka, na Israeli, uliowaapia kwa jina lako mwenyewe na kusema, ‘Nitaufanya uzao wenu uwe mwingi kama nyota za mbinguni,+ nami nitaupa uzao* wenu nchi yote hii niliyowaahidi, ili iwe miliki yao ya kudumu.’”+
14 Basi Yehova akaanza kufikiria upya* msiba ambao alikuwa amesema atawaletea watu wake.+
15 Kisha Musa akageuka na kushuka kutoka mlimani akiwa amebeba yale mabamba mawili ya Ushahidi+ mikononi mwake.+ Mabamba hayo yalikuwa yameandikwa pande zote mbili; upande wa mbele na wa nyuma. 16 Mabamba hayo yalitengenezwa na Mungu, na maandishi yake yalikuwa maandishi ya Mungu yalichongwa kwenye mabamba hayo.+ 17 Yoshua alipoanza kusikia sauti za watu wakipiga kelele, akamwambia Musa: “Kuna kelele za vita kambini.” 18 Lakini Musa akasema:
“Si sauti za watu wanaoimba kwa sababu ya ushindi,*
Wala si sauti za watu wanaolia kwa sababu ya kushindwa;
Ninasikia sauti za uimbaji wa aina nyingine.”
19 Mara tu Musa alipoikaribia kambi na kuona ile sanamu ya ndama+ na watu wakicheza dansi, akaanza kuwaka hasira, naye akayatupa chini yale mabamba mawili yaliyokuwa mikononi mwake, yakavunjika-vunjika chini ya mlima.+ 20 Akaichukua sanamu ya ndama waliyokuwa wametengeneza, akaiteketeza na kuipondaponda ikawa ungaunga;+ kisha akaunyunyiza juu ya maji na kuwalazimisha Waisraeli wayanywe.+ 21 Musa akamuuliza Haruni: “Watu hawa walikufanya nini hivi kwamba ukasababisha watende dhambi kubwa hivi?” 22 Haruni akajibu: “Usikasirike, bwana wangu. Unajua vizuri kwamba watu hawa wana mwelekeo wa kutenda maovu.+ 23 Basi waliniambia, ‘Tutengenezee mungu atakayetuongoza, kwa sababu hatujui lililompata huyu Musa, mtu aliyetuongoza kutoka katika nchi ya Misri.’+ 24 Basi nikawaambia, ‘Mtu yeyote aliye na dhahabu aitoe na kunipa.’ Kisha nikaitupa motoni na ndama huyu akatokea.”
25 Musa akaona kwamba watu wanafanya watakavyo, kwa sababu Haruni aliwaacha wafanye watakavyo, hivi kwamba wakajiletea aibu mbele ya wapinzani wao. 26 Kisha Musa akasimama kwenye lango la kambi na kusema: “Ni nani aliye upande wa Yehova? Njooni kwangu!”+ Ndipo Walawi wote wakakusanyika kumzunguka. 27 Basi Musa akawaambia: “Yehova Mungu wa Israeli amesema, ‘Kila mmoja wenu na ajifunge upanga wake na kupita kotekote kambini, kutoka lango mpaka lango, amuue ndugu yake, jirani yake, na rafiki yake wa karibu.’”+ 28 Walawi wakafanya kama Musa alivyowaambia. Kwa hiyo wanaume 3,000 hivi waliuawa siku hiyo. 29 Kisha Musa akawaambia: “Jitakaseni* leo kwa ajili ya Yehova, kwa maana kila mmoja wenu amemshambulia mwana wake mwenyewe na ndugu yake mwenyewe;+ atawabariki leo.”+
30 Siku iliyofuata, Musa akawaambia watu: “Mlitenda dhambi kubwa sana, na sasa nitapanda kwenda kwa Yehova ili nione ikiwa ninaweza kuomba msamaha kwa ajili ya dhambi yenu.”+ 31 Kwa hiyo Musa akarudi kwa Yehova na kumwambia: “Watu hawa wametenda dhambi kubwa sana! Walijitengenezea mungu wa dhahabu!+ 32 Lakini sasa ukipenda, wasamehe dhambi yao;+ la sivyo, tafadhali nifute katika kitabu chako ulichoandika.”+ 33 Hata hivyo, Yehova akamwambia Musa: “Yeyote aliyenitendea dhambi, nitamfuta katika kitabu changu. 34 Nenda sasa, waongoze watu kwenda mahali nilipokuambia. Tazama! Malaika wangu atakutangulia,+ na siku ya kuwaadhibu itakapofika, nitawaadhibu kwa sababu ya dhambi yao.” 35 Ndipo Yehova akaanza kuwaletea watu pigo kwa sababu walikuwa wametengeneza sanamu ya ndama, sanamu ambayo Haruni alitengeneza.
33 Yehova akaendelea kumwambia Musa: “Ondoka mahali hapa pamoja na watu uliowaongoza kutoka katika nchi ya Misri. Safirini mpaka nchi niliyomwapia Abrahamu, Isaka, na Yakobo, niliposema, ‘Nitaupa uzao wenu* nchi hii.’+ 2 Nitamtuma malaika awatangulie+ na kuwafukuza Wakanaani, Waamori, Wahiti, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi.+ 3 Pandeni mpaka kwenye nchi inayotiririka maziwa na asali.+ Lakini sitaenda pamoja nanyi, kwa sababu ninyi ni watu wakaidi, *+ na huenda nikawaangamiza kabisa njiani.”+
4 Watu waliposikia maneno hayo makali, wakaanza kuomboleza, na hakuna yeyote kati yao aliyevaa mapambo yake. 5 Yehova akamwambia Musa: “Waambie Waisraeli, ‘Ninyi ni watu wakaidi.*+ Ninaweza kupita mara moja katikati yenu na kuwaangamiza kabisa.+ Sasa basi, msivae mapambo yenu ninapofikiria nitakavyowatendea.’” 6 Kwa hiyo kuanzia Mlima Horebu na kuendelea, Waisraeli hawakuvaa* mapambo yao.
7 Sasa Musa akachukua hema lake na kulipiga nje ya kambi, mbali kidogo na kambi, naye akaliita hema la mkutano. Mtu yeyote aliyetafuta ushauri wa Yehova+ alikuwa akienda kwenye hema la mkutano, lililokuwa nje ya kambi. 8 Kila mara Musa alipokuwa akienda kwenye hema hilo, watu wote walitoka na kusimama kwenye milango ya mahema yao, nao walimtazama Musa mpaka alipoingia ndani ya hema hilo. 9 Kila mara Musa alipoingia katika hema hilo, ile nguzo ya wingu+ ilishuka chini na kusimama kwenye mlango wa hema hilo Mungu alipokuwa akiongea na Musa.+ 10 Watu wote walipoona nguzo hiyo ya wingu ikisimama kwenye mlango wa hema, kila mmoja wao alisimama na kuinama chini kwenye mlango wa hema lake. 11 Yehova aliongea na Musa uso kwa uso,+ kama mwanadamu anavyoongea na mwanadamu mwenzake. Musa aliporudi kambini, Yoshua+ mwana wa Nuni, aliyekuwa mhudumu na mtumishi wake,+ hakuondoka hemani.
12 Sasa Musa akamwambia Yehova: “Angalia, unaniambia, ‘Waongoze watu hawa,’ lakini hujaniambia ni nani utakayemtuma pamoja nami. Isitoshe umeniambia, ‘Ninakujua kwa jina* na umepata kibali machoni pangu.’ 13 Tafadhali, ikiwa nimepata kibali machoni pako, nifundishe njia zako+ ili nikujue na kuendelea kuwa na kibali machoni pako. Pia, kumbuka kwamba taifa hili ni watu wako.”+ 14 Basi akasema: “Mimi mwenyewe nitakwenda* pamoja nawe,+ nami nitakupumzisha.”+ 15 Kisha Musa akamwambia: “Ikiwa wewe mwenyewe huendi* pamoja nasi, usituondoe mahali hapa. 16 Itajulikanaje kwamba mimi nimepata kibali machoni pako, mimi na watu wako? Je, haitajulikana ukienda pamoja nasi,+ ili mimi na watu wako tuonekane kuwa tofauti na watu wengine wote duniani?”+
17 Yehova akaendelea kumwambia Musa: “Nitafanya pia jambo hilo unaloomba, kwa sababu umepata kibali machoni pangu nami nakujua wewe kwa jina.” 18 Ndipo Musa akasema: “Tafadhali nionyeshe utukufu wako.” 19 Lakini akamwambia: “Nitaufanya wema wangu wote upite mbele ya uso wako, nami nitatangaza jina langu Yehova mbele yako;+ nami nitamwonyesha kibali yule ninayetaka kumwonyesha kibali, nami nitamwonyesha rehema yule ninayetaka kumwonyesha rehema.”+ 20 Lakini akasema: “Huwezi kuuona uso wangu, kwa sababu hakuna mwanadamu anayeweza kuniona na aendelee kuishi.”
21 Yehova akaendelea kusema: “Kuna mahali hapa karibu nami. Simama juu ya mwamba. 22 Utukufu wangu utakapokuwa ukipita, nitakuingiza kwenye shimo ndani ya mwamba, nami nitakukinga kwa mkono wangu mpaka nitakapopita. 23 Kisha nitauondoa mkono wangu, nawe utauona mgongo wangu. Lakini uso wangu hautaonekana.”+
34 Kisha Yehova akamwambia Musa: “Jichongee mabamba mawili ya mawe kama yale ya kwanza,+ nami nitaandika kwenye mabamba hayo maneno yaliyokuwa kwenye yale mabamba ya kwanza+ uliyoyavunja.+ 2 Jitayarishe kwa ajili ya asubuhi, kwa maana asubuhi utapanda Mlima Sinai na kusimama huko mbele zangu juu ya mlima huo.+ 3 Lakini mtu yeyote asipande pamoja nawe, na mtu mwingine yeyote asionekane popote mlimani. Hata mifugo haipaswi kulisha mbele ya mlima huo.”+
4 Basi Musa akachonga mabamba mawili ya mawe kama yale ya kwanza, akaamka asubuhi na mapema na kupanda Mlima Sinai, kama Yehova alivyomwamuru, akayabeba yale mabamba mawili ya mawe mikononi mwake. 5 Ndipo Yehova akashuka+ katika wingu na kusimama pamoja naye huko na kutangaza jina lake, Yehova.+ 6 Yehova alipita mbele yake akitangaza: “Mimi Yehova, Yehova, ni Mungu mwenye rehema+ na huruma,*+ si mwepesi wa hasira,+ nina upendo mwingi mshikamanifu*+ na kweli,*+ 7 ninawatendea maelfu kwa upendo mshikamanifu,+ ninasamehe makosa na uovu na dhambi,+ lakini sikosi kamwe kuwaadhibu wenye hatia,+ ninawaadhibu wana na wajukuu kufikia kizazi cha tatu na cha nne kwa sababu ya makosa ya baba zao.”+
8 Musa akainama haraka mpaka chini na kusujudu. 9 Kisha akasema: “Ikiwa sasa nimepata kibali machoni pako, Ee Yehova, sasa tafadhali, Yehova, nenda pamoja nasi uwe kati yetu,+ ingawa sisi ni watu wakaidi,*+ utusamehe makosa yetu na dhambi zetu,+ nawe utuchukue kuwa mali yako mwenyewe.” 10 Naye akasema: “Tazama, ninafanya agano: Nitafanya mbele ya watu wako wote mambo yanayostaajabisha ambayo sijawahi kamwe kuyafanya* katika dunia yote wala kati ya mataifa yote,+ na watu wote mnaoishi miongoni mwao wataona kazi yangu mimi, Yehova, kwa sababu nitafanya jambo linaloogopesha kwa ajili yenu.+
11 “Sikilizeni mambo ninayowaamuru leo.+ Tazama, ninawafukuza Waamori, Wakanaani, Wahiti, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi+ kutoka mbele yenu. 12 Muwe waangalifu msifanye agano na wakaaji wa nchi mnayoenda kuingia,+ ili agano hilo lisiwe mtego kwenu.+ 13 Lakini mtabomoa madhabahu zao, mtazivunjavunja nguzo zao takatifu, na kuikata miti yao mitakatifu.*+ 14 Msimwinamie mungu mwingine,+ kwa sababu mimi Yehova ninajulikana kuwa Mungu ninayetaka* watu waniabudu mimi peke yangu.* Naam, mimi ni Mungu ninayetaka watu waniabudu mimi peke yangu.+ 15 Muwe waangalifu msifanye agano na wakaaji wa nchi, kwa maana wanapofanya ukahaba na miungu yao na kuitolea dhabihu,+ mmoja wao atawaalika nanyi mtakula dhabihu yake.+ 16 Kisha kwa hakika mtawachukua baadhi ya mabinti wao ili waolewe na wana wenu,+ na mabinti wao watafanya ukahaba na miungu yao na kusababisha wana wenu wafanye ukahaba na miungu yao.+
17 “Hampaswi kutengeneza miungu ya chuma.+
18 “Mnapaswa kuadhimisha Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu.+ Mtakula mikate isiyo na chachu, kama nilivyowaamuru; mtaila kwa siku saba wakati uliowekwa katika mwezi wa Abibu,*+ kwa sababu mlitoka Misri katika mwezi wa Abibu.
19 “Kila mzaliwa wa kwanza wa kiume* ni wangu,+ kutia ndani mifugo yenu yote, iwe ni ng’ombe dume wa kwanza au kondoo.+ 20 Mtamkomboa mzaliwa wa kwanza wa punda kwa kondoo. Lakini msipomkomboa, basi mtamvunja shingo. Mnapaswa kumkomboa kila mzaliwa wenu wa kwanza kati ya wana wenu.+ Mtu yeyote asije mbele zangu mikono mitupu.
21 “Kwa siku sita mtafanya kazi, lakini siku ya saba mtapumzika.*+ Mtapumzika hata wakati wa kulima na wa kuvuna.
22 “Nanyi mtafanya Sherehe yenu ya Majuma kwa kutumia mavuno ya kwanza ya ngano iliyokomaa, na pia Sherehe ya Kukusanya* mwishoni mwa mwaka.+
23 “Mara tatu kwa mwaka, wanaume wenu wote wanapaswa kwenda mbele za Bwana wa kweli, Yehova, Mungu wa Israeli.+ 24 Kwa maana nitayafukuza mataifa kutoka mbele yenu,+ nami nitapanua eneo lenu, na hakuna mtu atakayetamani nchi yenu mtakapokuwa mkipanda kwenda mbele za* Yehova Mungu wenu mara tatu kwa mwaka.
25 “Hampaswi kutoa damu ya dhabihu yangu pamoja na kitu chochote kilichotiwa chachu.+ Dhabihu ya sherehe ya Pasaka haipaswi kuhifadhiwa usiku kucha mpaka asubuhi.+
26 “Mazao bora ya kwanza yaliyokomaa* ya ardhi yenu mnapaswa kuyaleta katika nyumba ya Yehova Mungu wenu.+
“Msimchemshe mwanambuzi katika maziwa ya mama yake.”+
27 Yehova akaendelea kumwambia Musa: “Unapaswa kuandika maneno haya,+ kwa sababu kulingana na maneno haya, ninafanya agano pamoja nawe na pamoja na Israeli.”+ 28 Musa akaendelea kukaa huko pamoja na Yehova kwa siku 40, mchana na usiku. Hakula mkate wala kunywa maji.+ Naye Mungu aliandika kwenye yale mabamba, maneno ya agano hilo, zile Amri Kumi.*+
29 Basi Musa akashuka Mlima Sinai akiwa amebeba mikononi yale mabamba mawili+ ya Ushahidi. Aliposhuka mlimani, Musa hakujua kwamba ngozi ya uso wake ilikuwa ikitoa miale kwa sababu alikuwa ameongea na Mungu. 30 Haruni na Waisraeli wote walipomtazama Musa, waliona kwamba ngozi ya uso wake ilikuwa ikitoa miale, wakaogopa kumkaribia.+
31 Lakini Musa akawaita, kwa hiyo Haruni na wakuu wote wa kusanyiko wakamkaribia, naye Musa akaongea nao. 32 Baada ya hayo Waisraeli wote wakamkaribia, naye akawapa amri zote alizopewa na Yehova kwenye Mlima Sinai.+ 33 Musa alipomaliza kuongea nao, alikuwa akiufunika uso wake kwa kitambaa.+ 34 Lakini kila mara Musa alipoingia ndani mbele za Yehova ili kuongea naye, alikivua kitambaa hicho lakini alijifunika alipotoka nje.+ Alipotoka nje aliwajulisha Waisraeli amri zote alizopewa.+ 35 Nao Waisraeli waliona kwamba ngozi ya uso wa Musa ilitoa miale; basi Musa alijifunika tena kitambaa hicho usoni alipotoka na kukivua alipoingia kuzungumza na Mungu.+
35 Baadaye Musa akalikusanya pamoja kusanyiko lote la Waisraeli na kuliambia: “Haya ndiyo mambo ambayo Yehova ameamuru yafanywe:+ 2 Mtafanya kazi kwa siku sita, lakini siku ya saba itakuwa takatifu kwenu, ni sabato ya pumziko kamili kwa Yehova.+ Mtu yeyote atakayefanya kazi siku hiyo atauawa.+ 3 Hampaswi kuwasha moto katika makao yenu yoyote siku ya Sabato.”
4 Kisha Musa akaliambia kusanyiko lote la Waisraeli: “Yehova ameamuru hivi: 5 ‘Mtoleeni Yehova mchango kutoka miongoni mwenu.+ Kila mtu aliye na moyo wa kutoa kwa hiari+ na amletee Yehova mchango wa dhahabu, fedha, shaba, 6 nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, kitani bora, manyoya ya mbuzi,+ 7 ngozi za kondoo dume zilizotiwa rangi nyekundu, ngozi za sili, mbao za mshita, 8 mafuta kwa ajili ya taa, mafuta ya zeri ya kutengenezea mafuta yanayotumiwa kutia mafuta na uvumba uliotiwa manukato,+ 9 mawe ya shohamu, na mawe mengine ya kupambia efodi+ na kifuko cha kifuani.+
10 “‘Watu wote ambao ni stadi*+ kati yenu na waje kutengeneza kila kitu ambacho Yehova ameamuru, 11 yaani, hema la ibada na kifuniko chake, kulabu zake na viunzi vyake vya mbao, fito zake, nguzo zake, na vikalio vyake; 12 Sanduku la Agano+ na fito zake,+ kifuniko,+ na pazia+ linalofunika sanduku hilo; 13 meza+ na fito zake na vyombo vyake vyote na mikate ya wonyesho;+ 14 kinara cha taa+ na vyombo vyake na taa zake na mafuta yake;+ 15 madhabahu ya uvumba+ na fito zake; mafuta yanayotumiwa kutia mafuta na uvumba uliotiwa manukato;+ pazia la mlango wa hema la ibada; 16 madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa+ na wavu wake wa shaba, fito zake na vyombo vyake vyote; beseni na kinara chake;+ 17 mapazia ya ua yanayoning’inia,+ nguzo zake na vikalio vyake; pazia la mlango wa ua; 18 vigingi vya hema la ibada na vigingi vya ua na kamba zake;+ 19 mavazi yaliyofumwa kwa ustadi+ ya kuhudumu mahali patakatifu, mavazi matakatifu ya kuhani Haruni,+ na mavazi ya wanawe ya kutumikia wakiwa makuhani.’”
20 Kwa hiyo kusanyiko lote la Waisraeli likaondoka mbele ya Musa. 21 Basi kila mtu ambaye moyo wake ulimsukuma+ na kila mtu aliyechochewa na roho yake akaja na kumletea Yehova mchango ili utumiwe katika kazi ya hema la mkutano, yaani, katika utumishi wake wote, na kwa ajili ya mavazi matakatifu. 22 Nao wakaendelea kuja, wanaume pamoja na wanawake, kila mtu aliyekuwa na moyo wa kutoa kwa hiari akaleta bizimu, vipuli, pete, na vito vingine, kutia ndani vito vya dhahabu vya kila aina. Wote wakamletea Yehova matoleo yao* ya dhahabu.+ 23 Na wote waliokuwa na nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, kitani bora, manyoya ya mbuzi, ngozi za kondoo dume zilizotiwa rangi nyekundu, na ngozi za sili, wakaleta vitu hivyo. 24 Wote waliotoa fedha na shaba wakaleta mchango wa Yehova, na wote waliokuwa na mbao za mshita za kutumiwa katika kazi yoyote ile wakazileta.
25 Wanawake wote wenye ustadi+ wa kusokota wakasokota kwa mikono yao na kuleta vitu walivyosokota: nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora. 26 Na wanawake wote wenye ustadi ambao walisukumwa na mioyo yao wakasokota manyoya ya mbuzi.
27 Nao wakuu wakaleta mawe ya shohamu na mawe mengine ya kupambia efodi na kifuko cha kifuani,+ 28 na mafuta ya zeri na mafuta kwa ajili ya taa na ya kutumiwa kutengenezea mafuta ya kutia mafuta+ na kwa ajili ya uvumba uliotiwa manukato.+ 29 Wanaume na wanawake wote waliochochewa na mioyo yao wakaleta kitu fulani kwa ajili ya kazi ambayo Yehova alimwamuru Musa ifanywe; Waisraeli walimletea Yehova vitu hivyo vikiwa toleo la hiari.+
30 Kisha Musa akawaambia Waisraeli: “Tazameni, Yehova amemchagua Bezaleli mwana wa Uri mwana wa Huru wa kabila la Yuda.+ 31 Amemjaza roho ya Mungu, amempa hekima, uelewaji, na ujuzi katika kila aina ya ufundi 32 ili abuni kazi za usanii akitumia dhahabu, fedha, na shaba, 33 ili achonge na kupamba kwa mawe, na kutengeneza vifaa vya mbao vya kila aina kwa usanii. 34 Naye ameweka moyoni mwake ustadi wa kufundisha, yeye na Oholiabu+ mwana wa Ahisamaki wa kabila la Dani. 35 Amewajaza ustadi wa*+ kufanya kazi zote za ufundi, kutarizi, na kufuma kwa nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora, na kazi zote za mfumaji. Wanaume hao watafanya kazi za kila aina na kubuni vyombo vya kila aina kwa ufundi.
36 “Bezaleli atafanya kazi pamoja na Oholiabu na kila mtu mwenye ustadi* ambaye Yehova amempa hekima na uelewaji ili kujua jinsi ya kufanya utumishi wote mtakatifu kama Yehova alivyoamuru.”+
2 Kisha Musa akamwita Bezaleli na Oholiabu na kila mtu mwenye ustadi ambaye Yehova aliweka hekima moyoni mwake,+ kila mtu ambaye moyo wake ulimsukuma kujitolea kufanya kazi.+ 3 Basi wakachukua kutoka kwa Musa mchango wote+ ambao Waisraeli walileta kwa ajili ya utumishi mtakatifu. Hata hivyo, watu wakaendelea kumletea matoleo ya hiari, asubuhi baada ya asubuhi.
4 Walipoanza kufanya kazi takatifu, mafundi wote wenye ustadi wakaja, mmoja baada ya mwingine, 5 nao walikuwa wakimwambia Musa: “Watu wanaleta vitu vingi sana kuliko vinavyohitajika kwa ajili ya kazi ambayo Yehova ameamuru ifanywe.” 6 Kwa hiyo Musa akaamuru kwamba tangazo litolewe kotekote kambini, likisema: “Wanaume na wanawake, msilete vitu zaidi kwa ajili ya mchango mtakatifu.” Basi watu wakazuiwa wasilete tena kitu chochote. 7 Vitu walivyoleta vilitosha kukamilisha kazi yote iliyopaswa kufanywa, tena vilizidi.
8 Kwa hiyo mafundi wote stadi+ walitengeneza hema la ibada+ kwa vitambaa kumi vya kitani bora kilichosokotwa, kwa nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, na kitambaa cha rangi nyekundu; akavitarizi* kwa michoro ya makerubi.+ 9 Kila kitambaa cha hema la ibada kilikuwa na urefu wa mikono 28* na upana wa mikono 4. Vitambaa vyote vilikuwa na ukubwa uleule. 10 Akaviunganisha pamoja vitambaa vitano vya hema, na pia akaviunganisha pamoja vile vitambaa vingine vitano. 11 Kisha akatengeneza vitanzi vya nyuzi za bluu kwenye upindo wa kitambaa cha mwisho. Naye akafanya vivyo hivyo kwenye upindo wa kitambaa kile kingine cha mwisho mahali ambapo vingeunganishwa. 12 Akatengeneza vitanzi 50 kwenye kitambaa kimoja na vitanzi vingine 50 kwenye upindo wa kitambaa cha pili ili vitanzi hivyo vielekeane vinapounganishwa. 13 Hatimaye, akatengeneza vibanio 50 vya dhahabu na kuviunganisha vitambaa hivyo pamoja kwa vibanio hivyo, basi hema la ibada likawa na kitambaa kimoja kizima.
14 Kisha akatengeneza vitambaa vya manyoya ya mbuzi vya kufunika hema hilo. Akatengeneza vitambaa 11 vya hema.+ 15 Kila kitambaa kilikuwa na urefu wa mikono 30 na upana wa mikono 4. Vitambaa vyote 11 vilikuwa na ukubwa uleule. 16 Kisha akaunganisha vitambaa vitano pamoja na vile vitambaa vingine sita pamoja. 17 Halafu akatengeneza vitanzi 50 kwenye upindo wa kitambaa cha kwanza, kwenye kipande cha mwisho kabisa, na vitanzi 50 kwenye upindo wa kitambaa cha pili, mahali vinapounganishwa. 18 Naye akatengeneza vibanio 50 vya shaba vya kuunganisha hema pamoja ili liwe na kitambaa kimoja kizima.
19 Akatengeneza kifuniko cha hema kwa kutumia ngozi za kondoo dume zilizotiwa rangi nyekundu na juu yake kifuniko cha ngozi za sili.+
20 Kisha akatengeneza viunzi vya mbao za mshita+ vilivyo wima kwa ajili ya hema hilo.+ 21 Kila kiunzi kilikuwa na urefu wa mikono kumi na upana wa mkono mmoja na nusu. 22 Kila kiunzi kilikuwa na ndimi mbili* zilizounganishwa pamoja. Hivyo ndivyo alivyotengeneza viunzi vyote vya hema la ibada. 23 Kwa hiyo alitengeneza viunzi 20 kwa ajili ya upande wa kusini wa hema la ibada. 24 Kisha akatengeneza vikalio 40 vya fedha chini ya vile viunzi 20: vikalio viwili chini ya kiunzi kimoja pamoja na ndimi zake mbili na vikalio vingine viwili chini ya kila kiunzi kilichofuata pamoja na ndimi zake mbili.+ 25 Akatengeneza viunzi 20 upande wa pili wa hema, upande wa kaskazini 26 pamoja na vikalio vyake 40 vya fedha, vikalio viwili chini ya kiunzi kimoja na vikalio viwili chini ya kila kiunzi kilichofuata.
27 Akatengeneza viunzi sita sehemu ya nyuma ya hema la ibada, upande wa magharibi.+ 28 Naye akatengeneza viunzi viwili viwe mihimili miwili ya pembeni upande wa nyuma wa hema la ibada. 29 Katika pembe zote mbili kulikuwa na viunzi viwili kuanzia sehemu ya chini mpaka sehemu ya juu, kwenye pete ya kwanza. Hivyo ndivyo alivyotengeneza ile mihimili miwili ya pembeni. 30 Kwa ujumla kulikuwa na viunzi vinane na vikalio vyake 16 vya fedha, vikalio viwili chini ya kila kiunzi.
31 Kisha akatengeneza fito za mshita, fito tano kwa ajili ya viunzi vya upande mmoja wa hema la ibada+ 32 na fito tano kwa ajili ya viunzi vya upande wa pili wa hema la ibada na fito tano kwa ajili ya viunzi vya sehemu ya nyuma ya hema la ibada, upande wa magharibi. 33 Akatengeneza ufito katikati ya viunzi kutoka mwisho mmoja mpaka mwisho mwingine. 34 Akavifunika viunzi hivyo kwa dhahabu, akatengeneza pete za dhahabu ili zishikilie zile fito, naye akazifunika fito hizo kwa dhahabu.+
35 Kisha akatengeneza pazia+ la nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa. Akalitarizi+ kwa michoro ya makerubi.+ 36 Kisha akalitengenezea nguzo nne za mshita na kuzifunika kwa dhahabu, akatengeneza pia kulabu za dhahabu na vikalio vinne vya fedha kwa ajili ya nguzo hizo. 37 Halafu akatengeneza pazia la mlango wa hema kwa nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa na kufumwa,+ 38 na pia nguzo zake tano na vibanio vyake. Akafunika kwa dhahabu sehemu ya juu ya nguzo hizo pamoja na kulabu* zake, lakini vikalio vyake vitano vilikuwa vya shaba.
37 Kisha Bezaleli+ akatengeneza sanduku la agano+ kwa mbao za mshita. Lilikuwa na urefu wa mikono miwili na nusu* na upana wa mkono mmoja na nusu na kimo cha mkono mmoja na nusu.+ 2 Akalifunika ndani na nje kwa dhahabu safi na kutengeneza ukingo wa dhahabu kulizunguka.+ 3 Kisha akalitengenezea pete nne za dhahabu na kuzifunga sehemu ya juu ya miguu yake minne, pete mbili upande mmoja na pete mbili upande wa pili. 4 Halafu akatengeneza fito za mshita na kuzifunika kwa dhahabu.+ 5 Akazitia fito hizo kwenye zile pete zilizo pande mbili za Sanduku hilo ili zitumiwe kulibeba.+
6 Akatengeneza kifuniko cha dhahabu safi.+ Kilikuwa na urefu wa mikono miwili na nusu na upana wa mkono mmoja na nusu.+ 7 Kisha akatengeneza makerubi wawili+ wa dhahabu kwa nyundo kwenye miisho miwili ya kifuniko hicho.+ 8 Kerubi mmoja alikuwa kwenye mwisho mmoja, na yule kerubi mwingine kwenye mwisho wa pili wa kifuniko. Alitengeneza makerubi hao kwenye pande zote mbili za kifuniko. 9 Makerubi hao walikuwa wamenyoosha mabawa yao kuelekea juu, na hivyo kukifunika kifuniko hicho kwa mabawa yao.+ Walielekeana huku nyuso zao zikitazama kifuniko.+
10 Kisha akatengeneza meza ya mbao za mshita.+ Ilikuwa na urefu wa mikono miwili, upana wa mkono mmoja, na kimo cha mkono mmoja na nusu.+ 11 Akaifunika kwa dhahabu safi na kutengeneza ukingo wa dhahabu kuizunguka. 12 Kisha akatengeneza utepe wenye upana wa kiganja kimoja* kuizunguka na ukingo wa dhahabu kuzunguka utepe huo. 13 Pia, akaitengenezea pete nne za dhahabu na kuzitia kwenye pembe nne za miguu yake minne. 14 Pete hizo zilikuwa karibu na utepe ili fito za kubebea meza hiyo zitiwe humo. 15 Halafu akatengeneza fito za mshita na kuzifunika kwa dhahabu ili zitumiwe kubebea meza hiyo. 16 Baada ya hayo akatengeneza sahani, vikombe, magudulia, na mabakuli ya meza hiyo kwa dhahabu safi ili yatumiwe kumimina matoleo ya vinywaji.+
17 Halafu akatengeneza kinara cha taa kwa dhahabu safi.+ Alikitengeneza kinara hicho cha taa kwa nyundo. Sehemu yake ya chini, shina lake, matawi yake, vikombe vyake, matumba yake, na maua yake yalitengenezwa kwa kipande kimoja cha dhahabu.+ 18 Kinara hicho kilikuwa na matawi sita, matawi matatu upande mmoja na matawi matatu upande wa pili. 19 Kila tawi lilikuwa na vikombe vitatu vyenye umbo la maua ya mlozi, na kila kikombe kilikuwa na ua na tumba lake. Hivyo ndivyo matawi hayo sita yalivyotengenezwa kwenye shina la kinara hicho cha taa. 20 Shina la kinara lilikuwa na vikombe vinne vyenye umbo la maua ya mlozi, kila kikombe kilikuwa na ua na tumba lake. 21 Kulikuwa na tumba chini ya jozi ya kwanza ya matawi hayo sita, tumba chini ya jozi ya pili, na tumba chini ya jozi ya tatu. 22 Matumba na matawi yake na kinara chote cha taa kilitengenezwa kwa kipande kimoja cha dhahabu safi, kwa kutumia nyundo. 23 Kisha akatengeneza taa saba+ pamoja na koleo zake na vyetezo vyake kwa dhahabu safi. 24 Alitumia talanta moja* ya dhahabu safi kutengeneza kinara hicho na vifaa vyake vyote.
25 Kisha akatumia mbao za mshita kujenga madhabahu ya kufukizia uvumba.+ Ilikuwa ya mraba, yenye urefu wa mkono mmoja, upana wa mkono mmoja, na kimo cha mikono miwili. Pembe zake zilikuwa sehemu ya hiyo madhabahu.+ 26 Aliifunika kwa dhahabu safi sehemu yake ya juu, pande zote kuizunguka na pia pembe zake, na kutengeneza ukingo wa dhahabu kuizunguka. 27 Akaitengenezea pete mbili za dhahabu chini ya ukingo wake kwenye pande zake mbili zinazoelekeana ili zishikilie fito za kubebea madhabahu. 28 Baada ya hayo akatengeneza fito za mshita na kuzifunika kwa dhahabu. 29 Alitengeneza pia mafuta matakatifu ya kutia mafuta+ na uvumba safi uliotiwa manukato+ na kuchanganywa kwa ustadi.*
38 Akatumia mbao za mshita kutengeneza madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa. Ilikuwa ya mraba, yenye urefu wa mikono mitano,* upana wa mikono mitano, na kimo cha mikono mitatu.+ 2 Kisha akatengeneza pembe kwenye ncha zake nne. Pembe hizo zilikuwa sehemu ya hiyo madhabahu. Naye akaifunika kwa shaba.+ 3 Baada ya hayo akatengeneza vyombo vyote vya madhabahu: ndoo za kuondolea majivu, sepetu, mabakuli, nyuma,* na vyetezo. Alitengeneza vyombo hivyo vyote kwa shaba. 4 Pia, alitengeneza wavu wa shaba kwa ajili ya madhabahu, chini ya ukingo wake, katikati ya madhabahu. 5 Alitengeneza pete nne kwenye pembe nne za wavu huo karibu na wavu huo wa shaba, ili zishikilie fito. 6 Baada ya hayo akatengeneza fito kwa mbao za mshita na kuzifunika kwa shaba. 7 Kisha akazitia fito hizo kwenye zile pete zilizo kwenye pande za madhabahu ili zitumiwe kubebea madhabahu. Alitengeneza madhabahu hiyo kama sanduku la mbao lenye uwazi.
8 Kisha akatengeneza beseni la shaba+ na kinara chake cha shaba; alitumia vioo* vya wanawake waliotumikia kwenye mlango wa hema la mkutano kulingana na mpangilio uliowekwa.
9 Kisha akatengeneza ua.+ Upande wa kusini wa ua huo, alitengeneza mapazia yanayoning’inia ya kitani bora kilichosokotwa yenye urefu wa mikono 100.+ 10 Ulikuwa na nguzo 20 na vikalio 20 vya shaba, na kulabu za nguzo hizo na vitanzi* vyake vilikuwa vya fedha. 11 Pia, kulikuwa na mapazia yanayoning’inia upande wa kaskazini yenye urefu wa mikono 100. Nguzo zake 20 na vikalio vyake 20 vilikuwa vya shaba. Lakini kulabu za nguzo hizo na vitanzi* vyake vilikuwa vya fedha. 12 Hata hivyo, upande wa magharibi ulikuwa na mapazia yanayoning’inia yenye urefu wa mikono 50. Pia ulikuwa na nguzo kumi na vikalio kumi, kulabu na vitanzi* vyake vilikuwa vya fedha. 13 Ua huo ulikuwa na upana wa mikono 50 upande wa mashariki, yaani, upande wa mapambazuko ya jua. 14 Upande mmoja ulikuwa na mapazia yanayoning’inia yenye upana wa mikono 15, pamoja na nguzo tatu na vikalio vitatu. 15 Upande wa pili wa mlango wa ua ulikuwa na mapazia yanayoning’inia yenye upana wa mikono 15, pamoja na nguzo tatu na vikalio vyake vitatu. 16 Mapazia yote yanayoning’inia kuzunguka ua yalitengenezwa kwa kitani bora kilichosokotwa. 17 Vikalio vya nguzo vilikuwa vya shaba, kulabu za nguzo hizo na vitanzi* vyake vilikuwa vya fedha, sehemu za juu zilifunikwa kwa fedha, na nguzo zote za ua zilikuwa na kulabu za fedha.+
18 Pazia la mlango wa ua lilifumwa kwa nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa. Lilikuwa na urefu wa mikono 20 na kimo cha mikono 5, sawa na kimo cha mapazia ya ua yanayoning’inia.+ 19 Nguzo zake nne na vikalio vyake vinne vilikuwa vya shaba. Kulabu zake zilikuwa za fedha, na sehemu za juu za nguzo hizo pamoja na vitanzi* vilifunikwa kwa fedha. 20 Vigingi vyote vya hema la ibada na vya ua vilikuwa vya shaba.+
21 Ifuatayo ni orodha ya vitu vilivyotumiwa kutengeneza hema la ibada, yaani, hema la Ushahidi.+ Orodha hii ilitayarishwa kwa amri ya Musa, na lilikuwa jukumu la Walawi+ kuitayarisha chini ya uongozi wa Ithamari+ mwana wa Haruni kuhani. 22 Bezaleli+ mwana wa Uri mwana wa Huru wa kabila la Yuda alifanya mambo yote ambayo Yehova alimwamuru Musa. 23 Alikuwa pamoja na Oholiabu+ mwana wa Ahisamaki wa kabila la Dani, aliyekuwa fundi, mtarizi, na mfumaji wa nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora.
24 Dhahabu yote iliyotumiwa kwa kazi zote za mahali patakatifu ndiyo dhahabu yote iliyotolewa kama toleo la kutikiswa,+ ilikuwa talanta 29* na shekeli 730* kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu.* 25 Fedha iliyotolewa na wale walioandikishwa ilikuwa talanta 100 na shekeli 1,775 kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu.* 26 Nusu shekeli iliyotolewa na kila mwanamume ilikuwa nusu shekeli kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu,* ilitolewa na kila mwanamume aliyeandikishwa mwenye umri wa kuanzia miaka 20 na zaidi,+ wote walikuwa 603,550.+
27 Talanta 100 za fedha zilitumiwa kutengeneza vikalio vya mahali patakatifu na vikalio vya pazia; talanta 100 zilitumiwa kutengeneza vikalio 100, talanta moja kwa kila kikalio.+ 28 Alitumia zile shekeli 1,775 kutengeneza kulabu za nguzo na kufunika sehemu zake za juu na kuziunganisha pamoja.
29 Shaba iliyotolewa ikiwa toleo* ilikuwa talanta 70 na shekeli 2,400. 30 Alitumia shaba hiyo kutengeneza vikalio vya mlango wa hema la mkutano, madhabahu ya shaba na wavu wake wa shaba, vyombo vyote vya madhabahu, 31 vikalio vyote vya ua, vikalio vya mlango wa ua, vigingi vyote vya hema la ibada, na vigingi vyote+ vya ua.
39 Walitumia zile nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, na kitambaa cha rangi nyekundu+ kufuma kwa ustadi mavazi ya kuhudumu mahali patakatifu. Walimtengenezea Haruni mavazi matakatifu+ kama Yehova alivyomwamuru Musa.
2 Alitengeneza* efodi+ kwa dhahabu, nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa. 3 Walitengeneza mabamba membamba ya dhahabu kwa kutumia nyundo, naye akayakata yakawa nyuzi nyembamba ili zifumwe pamoja na zile nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora, akatarizi efodi. 4 Wakatengeneza vipande vya mabegani vilivyoungana, navyo vikaunganishwa kwenye miisho miwili ya efodi. 5 Mshipi uliofumwa unaoshikilia kwa nguvu efodi ulitengenezwa kwa vitu hivyohivyo,+ yaani, dhahabu, nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa, kama Yehova alivyomwamuru Musa.
6 Kisha wakatia mawe ya shohamu katika vifuko vya dhahabu na kuchonga majina ya wana wa Israeli kwenye mawe hayo, kama mtu anavyochonga muhuri.+ 7 Akayaweka mawe hayo kwenye vipande vya mabegani vya efodi, ili yawe mawe ya ukumbusho kwa wana wa Israeli,+ kama Yehova alivyomwamuru Musa. 8 Kisha akatengeneza kifuko cha kifuani+ na kukitarizi. Akakitengeneza kama efodi kwa kutumia dhahabu, nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa.+ 9 Kifuko hicho kilikuwa cha mraba kilipokunjwa mara mbili. Walikitengeneza kifuko hicho cha kifuani kikiwa na urefu wa shubiri moja* na upana wa shubiri moja kinapokunjwa mara mbili. 10 Wakaweka kwenye kifuko hicho mawe yaliyopangwa katika safu nne. Safu ya kwanza ilikuwa na zabarijadi, topazi, na zumaridi. 11 Safu ya pili ilikuwa na feruzi, yakuti, na yaspi. 12 Safu ya tatu ilikuwa na jiwe la leshemi,* akiki, na amethisti. 13 Safu ya nne ilikuwa na krisolito, shohamu, na yashefi. Mawe hayo yaliwekwa kwenye vifuko vya dhahabu. 14 Yalilingana na majina 12 ya wana wa Israeli, na majina hayo yalichongwa kama muhuri, na kila jina liliwakilisha mojawapo ya makabila 12 ya wana wa Israeli.
15 Kisha wakakitengenezea kifuko cha kifuani minyororo iliyosokotwa, kama kamba za dhahabu safi.+ 16 Halafu wakatengeneza vifuko viwili vya dhahabu na pete mbili za dhahabu na kuzitia kwenye pembe mbili za juu za kifuko hicho. 17 Baada ya hayo wakatia zile kamba mbili za dhahabu katika pete mbili zilizo kwenye pembe hizo. 18 Kisha wakatia ncha mbili za hizo kamba mbili katika vile vifuko viwili vya mabegani na kuzifunga ncha hizo kwenye vipande viwili vya efodi, sehemu ya mbele. 19 Halafu wakatengeneza pete mbili za dhahabu na kuziweka kwenye pembe mbili za chini, upande wa ndani wa kifuko cha kifuani, upande wa efodi.+ 20 Kisha wakatengeneza pete nyingine mbili za dhahabu upande wa mbele wa efodi, chini ya vipande viwili vya mabegani vya efodi, karibu na mahali inapoungana, juu ya mshipi uliofumwa wa efodi. 21 Hatimaye, wakafunga pete za kifuko cha kifuani pamoja na pete za efodi kwa kamba ya bluu, ili kifuko cha kifuani kibaki mahali pake kwenye efodi, juu ya mshipi uliofumwa, kama Yehova alivyomwamuru Musa.
22 Kisha akafuma joho lisilo na mikono la efodi kwa nyuzi za bluu peke yake.+ 23 Lilikuwa na nafasi ya kupitishia kichwa katikati sehemu ya juu. Sehemu hiyo ilikuwa na ukingo kuizunguka kama wa koti la vita, ili isiraruke. 24 Halafu wakatengeneza kwenye upindo wa joho hilo makomamanga ya nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, na kitambaa cha rangi nyekundu; vitu vyote hivyo vilisokotwa pamoja. 25 Walitengeneza kengele za dhahabu safi na kuzitia kati ya makomamanga kwenye upindo wote wa joho hilo lisilo na mikono; 26 walitia kengele kisha komamanga, kengele kisha komamanga kwenye upindo wote wa joho hilo lisilo na mikono lililotumiwa kuhudumu, kama Yehova alivyomwamuru Musa.
27 Pia walifuma kanzu za kitani bora kwa ajili ya Haruni na wanawe,+ 28 na pia kilemba+ cha kitani bora, kofia maridadi za kitani bora,+ suruali fupi*+ za kitani bora kilichosokotwa, 29 na ukumbuu uliofumwa kwa kitani bora kilichosokotwa, nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, na kitambaa cha rangi nyekundu, kama Yehova alivyomwamuru Musa.
30 Hatimaye, walitengeneza kwa dhahabu safi bamba linalong’aa, yaani, ile ishara takatifu ya wakfu,* na kuchonga maneno haya juu yake kama muhuri unavyochongwa: “Utakatifu ni wa Yehova.”+ 31 Wakalifunga bamba hilo kwa kamba ya bluu ili waliweke juu ya kilemba, kama Yehova alivyomwamuru Musa.
32 Basi wakakamilisha kazi yote ya hema la ibada, yaani, hema la mkutano; Waisraeli walifanya kila jambo ambalo Yehova alimwamuru Musa.+ Hivyo ndivyo walivyofanya.
33 Wakamletea Musa hema la ibada+ pamoja na vifaa vyake vyote: vibanio vyake,+ viunzi vyake,+ fito zake,+ nguzo zake na vikalio vyake;+ 34 kifuniko chake cha ngozi za kondoo dume zilizotiwa rangi nyekundu,+ kifuniko chake cha ngozi za sili, na pazia lake;+ 35 sanduku la ushahidi pamoja na fito zake+ na kifuniko chake;+ 36 meza, vyombo vyake vyote+ na mikate ya wonyesho; 37 kinara cha taa cha dhahabu safi, taa zake,+ safu zake za taa, na vyombo vyake vyote+ na mafuta kwa ajili ya taa hizo;+ 38 madhabahu+ ya dhahabu, mafuta yanayotumiwa kutia mafuta,+ uvumba uliotiwa manukato,+ pazia la mlango+ wa hema; 39 madhabahu ya shaba+ na wavu wake wa shaba, fito zake,+ vyombo vyake vyote,+ beseni na kinara chake;+ 40 mapazia ya ua yanayoning’inia, nguzo zake na vikalio vyake,+ pazia la mlango+ wa ua, kamba na vigingi vya hema+ na vifaa vyote vya utumishi wa hema la ibada, yaani, hema la mkutano; 41 yale mavazi yaliyofumwa kwa ustadi ya kuhudumu mahali patakatifu, mavazi matakatifu ya kuhani Haruni,+ na mavazi ya wanawe ya kutumikia wakiwa makuhani.
42 Waisraeli walifanya kazi yote kama Yehova alivyomwamuru Musa.+ 43 Musa alipokagua kazi yao yote, aliona kwamba walikuwa wameifanya kama Yehova alivyoamuru; basi Musa akawabariki.
40 Kisha Yehova akamwambia Musa: 2 “Siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, utajenga hema la ibada, yaani, hema la mkutano.+ 3 Weka sanduku la Ushahidi ndani yake,+ na ulifunike sanduku hilo kwa pazia.+ 4 Ingiza meza+ na upange vyombo vyake juu yake, kisha ulete kinara cha taa+ na kuwasha taa zake.+ 5 Halafu uweke madhabahu ya dhahabu ya kufukizia uvumba+ mbele ya sanduku la Ushahidi na kuweka pazia la mlango wa hema la ibada.+
6 “Utaweka madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa+ mbele ya mlango wa hema la ibada, yaani, hema la mkutano, 7 na kuweka beseni kati ya hema la mkutano na madhabahu, kisha utie maji ndani ya beseni hilo.+ 8 Halafu utengeneze ua+ kuzunguka hema hilo na kuweka pazia+ kwenye mlango wa ua. 9 Kisha uchukue mafuta yanayotumiwa kutia mafuta+ na kulitia mafuta hema la ibada na vitu vyote vilivyomo,+ nawe ulitakase pamoja na vyombo vyake vyote, ili liwe takatifu. 10 Utatia mafuta madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa pamoja na vyombo vyake vyote na kuitakasa, ili iwe madhabahu takatifu zaidi.+ 11 Nawe ulitie mafuta beseni na kinara chake na kulitakasa.
12 “Kisha mlete Haruni na wanawe karibu na mlango wa hema la mkutano na kuwaosha kwa maji.+ 13 Utamvisha Haruni mavazi matakatifu+ na kumtia mafuta+ na kumtakasa, naye atanitumikia akiwa kuhani. 14 Baada ya hayo walete wanawe karibu na kuwavisha kanzu.+ 15 Utawatia mafuta kama ulivyomtia mafuta baba yao,+ ili wanitumikie wakiwa makuhani, nao wataendelea kuwa makuhani daima katika vizazi vyao vyote kwa sababu wametiwa mafuta.”+
16 Musa alifanya yote ambayo Yehova alimwamuru.+ Hivyo ndivyo alivyofanya.
17 Katika mwezi wa kwanza, mwaka wa pili, siku ya kwanza ya mwezi, hema la ibada lilitengenezwa.+ 18 Musa alitengeneza hema la ibada kwa kuweka chini vikalio vyake,+ kuweka viunzi vyake,+ kuweka fito zake,+ na kusimamisha nguzo zake. 19 Akatandaza kitambaa cha hema+ juu ya viunzi vya hema hilo na kuweka kifuniko+ juu yake, kama Yehova alivyomwamuru Musa.
20 Kisha akachukua yale mabamba ya Ushahidi+ na kuyaweka ndani ya sanduku la Ushahidi,+ akatia fito+ kwenye pete za Sanduku hilo na kuweka kifuniko+ juu ya Sanduku hilo.+ 21 Akaingiza sanduku la Ushahidi ndani ya hema la ibada na kuweka pazia+ ambalo lilifunika sanduku la Ushahidi,+ kama Yehova alivyomwamuru Musa.
22 Kisha akaweka meza+ ndani ya hema la mkutano upande wa kaskazini, nje ya pazia, 23 naye akapanga juu yake ile mikate+ kwa safu mbele za Yehova, kama Yehova alivyomwamuru Musa.
24 Akaweka kile kinara cha taa+ ndani ya hema la mkutano mbele ya meza hiyo, upande wa kusini. 25 Kisha akawasha zile taa+ mbele za Yehova, kama Yehova alivyomwamuru Musa.
26 Halafu akaweka ile madhabahu ya dhahabu+ ndani ya hema la mkutano mbele ya pazia, 27 ili afukize juu yake uvumba+ uliotiwa manukato,+ kama Yehova alivyomwamuru Musa.
28 Kisha akaweka pazia+ la mlango wa hema la ibada.
29 Akaweka madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa+ kwenye mlango wa hema la ibada, yaani, hema la mkutano, ili atoe juu yake dhabihu za kuteketezwa+ na matoleo ya nafaka, kama Yehova alivyomwamuru Musa.
30 Kisha akaweka beseni kati ya hema la mkutano na madhabahu na kutia maji ndani yake ili makuhani wanawe+ mikono na miguu yao. 31 Musa na pia Haruni na wanawe walitumia maji ya beseni hilo kunawa mikono na miguu yao. 32 Kila mara walipoenda kwenye hema la mkutano au kukaribia madhabahu, walinawa+ mikono na miguu yao, kama Yehova alivyomwamuru Musa.
33 Mwishowe akatengeneza ua+ kuzunguka hema la ibada na ile madhabahu na kuweka pazia la mlango wa ua.+
Basi Musa akakamilisha kazi yote. 34 Ndipo wingu likaanza kufunika hema la mkutano, na utukufu wa Yehova ukajaa katika hema la ibada.+ 35 Musa alishindwa kuingia ndani ya hema la mkutano kwa sababu wingu liliendelea kulifunika, na utukufu wa Yehova ukajaa katika hema hilo.+
36 Kila mara wingu lilipoinuka kutoka juu ya hema la ibada, Waisraeli walivunja kambi katika hatua zote za safari yao.+ 37 Hata hivyo, wingu lilipokosa kuinuka, hawakuvunja kambi mpaka siku lilipoinuka.+ 38 Katika hatua zote za safari yao, Waisraeli wote waliona wingu la Yehova likiwa juu ya hema la ibada wakati wa mchana, na moto ukiwa juu yake wakati wa usiku.+
Tnn., “Na wote waliotoka katika kiuno cha Yakobo.”
Tnn., “wana wa Israeli.”
Au “wasimamizi wa kazi.”
Au “safina; sanduku.”
Maana yake “Aliyetolewa,” yaani, aliyeokolewa kutoka katika maji.
Au “Musa alipokuwa akipata nguvu.”
Au “akawatetea.”
Yaani, Yethro.
Maana yake “Mkaaji Mgeni Huko.”
Tnn., “siku nyingi.”
Au “mtaniabudu.”
Au “Ninachotaka.”
Au “Nitathibitika Kuwa Kile Nitakachothibitika Kuwa.” Angalia Nyongeza A4.
Tnn., “nina kinywa kizito.”
Tnn., “nitakuwa na kinywa chako.”
Au “atakuona kuwa mwakilishi wa Mungu.”
Au “waliokuwa wakiitafuta nafsi yako.”
Au “kisu cha jiwe gumu.”
Labda ni miguu ya malaika.
Au “mkabebe mizigo yenu.”
Au “ni wavivu.”
Au “Ninyi ni wavivu.”
Au “ninyi ni wavivu.”
Au “mmefanya tunuke uvundo mbele ya Farao na watumishi wake.”
Au “wenye nguvu.”
Tnn., “niliyoinua mkono wangu.”
Tnn., “mtu ambaye hajatahiriwa midomo?”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Tnn., “kulingana na majeshi yao.”
Tnn., “sijatahiriwa midomo.”
Tnn., “nimekufanya Mungu.”
Tnn., “majeshi yangu.”
Au “ufundi wao wa uchawi.”
Yaani, mifereji ya Mto Nile.
Au “mabakuli yenu ya.”
Aina ya mbu anayeitwa hak·kin·nam’ katika Kiebrania.
Aina ya nzi anayeuma.
Au “kutuhadaa.”
Au “kalibu.”
Au “kalibu.”
Au “umefagiliwa.”
Labda ni radi kubwa.
Aina fulani ya ngano ya hali ya chini iliyopandwa nchini Misri.
Au “majira yake yalichelewa.”
Tnn., “kuwa mtego kwetu.”
Inaelekea ni Musa.
Tnn., “Hatutaacha ukwato wowote.”
Tnn., “atakayeunoa ulimi wake dhidi ya.”
Tnn., “atagawana na jirani yake.”
Au “nafsi.”
Tnn., “katikati ya zile jioni mbili.”
Tnn., “mkiwa mmevifunga viuno vyenu.”
Tnn., “majeshi yenu.”
Yaani, wanakondoo au wanambuzi.
Tnn., “maangamizi yaingie.”
Tnn., “katika nyumba ya tangi la maji.”
Au “mabakuli yao ya.”
Yaani, kundi kubwa lenye mchanganyiko wa watu ambao hawakuwa Waisraeli, kutia ndani Wamisri.
Tnn., “majeshi yote ya.”
Tnn., “majeshi yao.”
Tnn., “Niwekee kando; Nitengee.”
Angalia Nyongeza B15.
Tnn., “katika mipaka yenu yote.”
Tnn., “katikati ya macho yako.”
Tnn., “kila kifungua mimba.”
Tnn., “kila kifungua mimba.”
Tnn., “katikati ya macho yako.”
Tnn., “kwa mkono ulioinuliwa.”
Yaani, kuanzia saa 8 hivi usiku hadi saa 12 asubuhi.
Tnn., “mkono wenye nguvu ambao.”
“Yah” ni ufupisho wa jina Yehova.
Tnn., “uchungu wa kuzaa.”
Shehe alikuwa mkuu wa kabila.
Au “watawala wa mabavu.”
Maana yake “Uchungu.”
Tnn., “Katikati ya zile jioni mbili.”
Karibu lita 2.2. Angalia Nyongeza B14.
Au “mwadhimisho wa sabato.”
Au “wakapumzika.”
Labda linatokana na neno la Kiebrania linalomaanisha “Ni nini hiki?”
Vitu muhimu vilihifadhiwa katika sanduku hili.
Efa ilikuwa sawa na lita 22 au kilogramu 13 hivi. Angalia Nyongeza B14.
Maana yake “Kujaribu; Jaribu.”
Maana yake “Kugombana.”
Au “kikumbusho.”
Maana yake “Yehova Ni Nguzo Yangu ya Ishara.”
Maana yake “Mkaaji Mgeni Huko.”
Maana yake “Mungu Wangu Ni Msaidizi.”
Tnn., “kutoka mkononi mwa Misri.”
Tnn., “kila wakati.”
Au “mali yangu ninayothamini sana.”
Labda angechomwa kwa mkuki.
Tnn., “Msimkaribie mwanamke.”
Au “kalibu.”
Au “na kuniasi mimi.” Tnn., “dhidi ya uso wangu.”
Au “umbo la.”
Tnn., “malango.”
Au “matoleo yenu ya amani.”
Au “yaliyochongwa.”
Tnn., “uchi wenu usionekane.”
Tnn., “Haya ndiyo maamuzi ya hukumu utakayowapa.”
Tnn., “akombolewe.”
Au labda, “kwa kifaa.”
Tnn., “na watoto wake watoke tumboni.”
Au “na kusiwepo na majeraha mabaya.”
Au “nafsi kwa nafsi.”
Au “ridhaa.”
Au “nafsi yake.”
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Au “mla riba.”
Au “rehani.”
Tnn., “ngozi yake.”
Au “neema.”
Au “mtawala.”
Yaani, mashinikizo ya mafuta na mashinikizo ya divai.
Au “ushahidi unaoungwa mkono na wengi.”
Tnn., “neno.”
Au “sitamwondolea mashtaka mtu mwovu.”
Au “Mnajua maisha (nafsi) ya mgeni.”
Tnn., “kinywani.”
Angalia Nyongeza B15.
Pia inaitwa Sherehe ya Majuma, au Pentekoste.
Au “mazao ya kwanza yaliyokomaa.”
Pia inaitwa Sherehe ya Vibanda (Mahema).
Au “matunda ya kwanza bora yaliyoiva.”
Au “nitafanya idadi ya siku zenu iwe kamili.”
Au “nitawafanya maadui wenu wote wawageuzie mgongo.”
Au labda, “washikwe na wasiwasi; waogope.”
Tnn., “maamuzi yote ya hukumu.”
Au “sufu iliyotiwa rangi ya zambarau.”
Rangi hiyo ilitoka kwa mdudu anayeitwa kochinili.
Mnyama wa baharini.
Au “nitapiga hema.”
Au “mchoro nitakaowaonyesha.”
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Karibu sentimita 7.4 (inchi 2.9). Angalia Nyongeza B14.
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Au “mchoro ulioonyeshwa.”
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Au “mihimili miwili.”
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Au “majivu yenye mafuta,” yaani, majivu yaliyojaa mafuta ya dhabihu.
Wingi wa kifaa kinachoitwa uma.
Au “pete; vitanzi; vibanio” vya kushikia.
Au “pete; vitanzi; vibanio” vya kushikia.
Au “wenye hekima moyoni.”
Yaani, upana wa kiganja cha mkono kuanzia kidole gumba hadi kidole kidogo, karibu sentimita 22.2 (inchi 8.75). Angalia Nyongeza B14.
Jiwe la thamani ambalo jina lake halijatajwa, huenda ni jiwe la kaharabu, hayasinthi, opali, au tumalini.
Angalia Kamusi.
Tnn., “na kuijaza mikono yao.”
Au “nguo za ndani.”
Tnn., “mbegu yake.”
Au “lile taji takatifu.”
Tnn., “Hivyo ndivyo utakavyoujaza mkono wa Haruni na mikono ya wanawe.”
Au “inayomtuliza.”
Au “inayomtuliza.”
Tnn., “ili kuijaza mikono yao.”
Tnn., “mgeni,” yaani, mtu ambaye si wa familia ya Haruni.
Tnn., “kuijaza mikono yao.”
Tnn., “katikati ya zile jioni mbili.”
Efa ilikuwa sawa na lita 22 au kilogramu 13 hivi. Angalia Nyongeza B14.
Hini ilikuwa sawa na lita 3.67. Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “katikati ya zile jioni mbili.”
Au “inayotuliza.”
Au “Nitapiga hema.”
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “Katikati ya zile jioni mbili.”
Au “uhai wake.”
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Au “shekeli takatifu.”
Gera moja ilikuwa na uzito wa gramu 0.57. Angalia Nyongeza B14.
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “kwa ajili ya uhai wenu.”
Au “uhai wenu.”
Au “shekeli takatifu.”
Hini ilikuwa sawa na lita 3.67. Angalia Nyongeza B14.
Au “kama anavyofanya mtengenezaji wa manukato.”
Tnn., “mgeni,” yaani, mtu ambaye si wa familia ya Haruni.
Au “kama anavyofanya mtengenezaji wa manukato.”
Tnn., “nimemwita kwa jina.”
Au “wenye hekima moyoni.”
Au “sanamu ya kuyeyushwa.”
Au “wamejichafua.”
Au “sanamu ya kuyeyushwa.”
Tnn., “wana shingo ngumu.”
Tnn., “akautuliza uso wa.”
Au “ughairi kuhusu.”
Tnn., “mbegu.”
Au “kughairi kuhusu.”
Au “tendo la kishujaa.”
Tnn., “Ujazeni mkono wenu.”
Tnn., “Nitaipa mbegu yenu.”
Au “wenye shingo ngumu.”
Tnn., “wenye shingo ngumu.”
Tnn., “waliyavua kabisa.”
Au “Nimekuchagua.”
Tnn., “Uso wangu utaenda.”
Tnn., “Ikiwa uso wako hauendi.”
Au “neema.”
Au “fadhili zenye upendo.”
Au “uaminifu.”
Au “wenye shingo ngumu.”
Au “kuyaumba.”
Angalia Kamusi.
Tnn., “Yehova, jina langu linadai.”
Au “nisiyevumilia washindani.”
Angalia Nyongeza B15.
Tnn., “Kila kifungua mimba.”
Au “mtashika sabato.”
Pia inaitwa Sherehe ya Vibanda (Mahema).
Tnn., “kuuona uso wa.”
Au “Matunda ya kwanza bora yaliyoiva.”
Tnn., “yale Maneno Kumi.”
Au “wenye hekima moyoni.”
Au “matoleo yao ya kutikiswa.”
Au “hekima moyoni ya.”
Au “mwenye hekima moyoni.”
Inaonekana ni Bezaleli.
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Au “mihimili miwili.”
Au “pete; vitanzi; vibanio” vya kushikia.
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Karibu sentimita 7.4 (inchi 2.9). Angalia Nyongeza B14.
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Au “kama anavyofanya mtengenezaji wa manukato.”
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Wingi wa kifaa kinachoitwa uma.
Yaani, vioo vya shaba vilivyong’arishwa sana.
Au “pete; vitanzi; vibanio” vya kushikia.
Au “pete; vitanzi; vibanio” vya kushikia.
Au “pete; vitanzi; vibanio” vya kushikia.
Au “pete; vitanzi; vibanio” vya kushikia.
Au “pete; vitanzi; vibanio” vya kushikia.
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Au “shekeli takatifu.”
Au “shekeli takatifu.”
Au “shekeli takatifu.”
Au “toleo la kutikiswa.”
Inaelekea ni Bezaleli.
Yaani, upana wa kiganja cha mkono kuanzia kidole gumba hadi kidole kidogo, karibu sentimita 22.2 (inchi 8.75). Angalia Nyongeza B14.
Jiwe la thamani ambalo halijulikani, huenda ni jiwe la kaharabu, hayasinthi, opali, au tumalini.
Au “nguo za ndani.”
Au “taji takatifu.”