Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt Mwanzo 1:1-50:26
  • Mwanzo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mwanzo
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Mwanzo

MWANZO

1 Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.+

2 Sasa dunia haikuwa na umbo nayo ilikuwa tupu,* na giza lilikuwa juu ya kilindi cha maji,*+ na nguvu ya utendaji ya Mungu*+ ilikuwa ikienda huku na huku juu ya maji.+

3 Na Mungu akasema: “Kuwe na nuru.” Basi kukawa na nuru.+ 4 Baada ya hayo, Mungu akaona kwamba nuru ilikuwa nzuri, na Mungu akaanza kuitenganisha nuru na giza. 5 Mungu akaiita nuru Mchana, lakini giza akaliita Usiku.+ Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya kwanza.

6 Kisha Mungu akasema: “Na kuwe na anga+ katikati ya maji, na anga liyatenganishe maji na maji.”+ 7 Ndipo Mungu akatengeneza anga na kuyatenganisha maji yaliyo chini ya anga na maji yaliyo juu ya anga.+ Na ikawa hivyo. 8 Mungu akaiita anga Mbingu. Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya pili.

9 Kisha Mungu akasema: “Maji yaliyo chini ya mbingu na yakusanyike mahali pamoja, na nchi kavu itokee.”+ Na ikawa hivyo. 10 Mungu akaiita nchi kavu Dunia,+ lakini mkusanyiko wa maji, akauita Bahari.+ Na Mungu akaona kuwa ni vyema.+ 11 Kisha Mungu akasema: “Dunia na ichipushe majani, mimea inayozaa mbegu na miti ya matunda inayozaa matunda kulingana na aina zake, miti inayozaa matunda yenye mbegu duniani.” Na ikawa hivyo. 12 Dunia ikaanza kuchipusha majani, mimea inayozaa mbegu+ na miti inayozaa matunda yenye mbegu, kulingana na aina zake. Kisha Mungu akaona kuwa ni vyema. 13 Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya tatu.

14 Kisha Mungu akasema: “Na kuwe na mianga*+ katika anga la mbingu ili itenganishe mchana na usiku,+ nayo itakuwa ishara ya kuonyesha majira na siku na miaka.+ 15 Itakuwa mianga katika anga la mbingu ili kuangazia dunia.” Na ikawa hivyo. 16 Ndipo Mungu akatengeneza mianga miwili mikubwa, mwanga mkubwa zaidi wa kutawala mchana+ na mwanga mdogo wa kutawala usiku, na pia nyota.+ 17 Basi Mungu akaiweka katika anga la mbingu ili iangazie dunia 18 na kutawala wakati wa mchana na wakati wa usiku na kutenganisha nuru na giza.+ Mungu akaona kuwa ni vyema. 19 Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya nne.

20 Kisha Mungu akasema: “Maji na yajae viumbe walio* hai, na viumbe wanaoruka waruke juu ya dunia katika anga la mbingu.”*+ 21 Mungu akaumba viumbe wakubwa* wa baharini na viumbe wote walio hai waendao na waliojaa majini kulingana na aina zao na kila kiumbe mwenye mabawa anayeruka, kulingana na aina yake. Mungu akaona kuwa ni vyema. 22 Basi Mungu akawabariki akisema: “Zaeni, muwe wengi na kujaza maji ya bahari,+ na viumbe wanaoruka wawe wengi duniani.” 23 Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya tano.

24 Kisha Mungu akasema: “Dunia na itokeze viumbe walio* hai kulingana na aina zao, wanyama wa kufugwa na wanyama wanaotambaa* na wanyama wa mwituni kulingana na aina zao.”+ Na ikawa hivyo. 25 Kisha Mungu akaumba wanyama wa mwituni kulingana na aina zao na wanyama wa kufugwa kulingana na aina zao na wanyama wote wanaotambaa kulingana na aina zao. Mungu akaona kuwa ni vyema.

26 Kisha Mungu akasema: “Na tufanye+ mtu kwa mfano+ wetu, kulingana na sura+ yetu, nao watawale samaki wa baharini na viumbe wanaoruka angani na wanyama wa kufugwa na dunia yote na kila mnyama anayetambaa duniani.”+ 27 Basi Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanamume na mwanamke aliwaumba.+ 28 Zaidi ya hilo, Mungu akawabariki, na Mungu akawaambia: “Zaeni, muwe wengi, muijaze dunia+ na kuitiisha,+ na mtawale+ samaki wa baharini na viumbe wanaoruka angani na kila kiumbe aliye hai anayetembea duniani.”

29 Kisha Mungu akasema: “Tazama nimewapa kila mmea duniani pote unaozaa mbegu na kila mti unaozaa matunda yenye mbegu. Itakuwa chakula chenu.+ 30 Na kila mnyama wa mwituni na kila kiumbe anayeruka angani na kila kiumbe mwenye uhai* anayetembea duniani, nimempa mimea yote ya kijani iwe chakula+ chake.” Ikawa hivyo.

31 Baada ya hayo Mungu akaona kila kitu alichoumba, na tazama! kilikuwa chema sana.+ Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya sita.

2 Basi mbingu na dunia na kila kitu kilichomo vikakamilika.*+ 2 Na kufikia siku ya saba, Mungu alikuwa amemaliza kazi aliyokuwa akifanya, naye akaanza kupumzika siku ya saba kutoka katika kazi yake yote aliyokuwa amefanya.+ 3 Na Mungu akaibariki siku ya saba na kuitangaza kuwa takatifu, kwa kuwa katika siku hiyo Mungu amekuwa akipumzika kutokana na kazi yake yote ya kuumba, vyote alivyokusudia kuumba.

4 Hii ndiyo historia ya mbingu na dunia wakati zilipoumbwa, siku ambayo Yehova* Mungu aliumba dunia na mbingu.+

5 Dunia bado haikuwa na kichaka chochote na hakuna mmea wowote uliokuwa umeanza kuchipuka, kwa sababu Yehova Mungu hakuwa amefanya mvua inyeshe duniani na hapakuwa na mtu wa kuilima ardhi. 6 Lakini ukungu ulikuwa ukipanda kutoka duniani, nao uliinywesha ardhi yote.

7 Kisha Yehova Mungu akamuumba mtu kutokana na mavumbi+ ya ardhi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai,+ na mtu huyo akawa mtu aliye hai.*+ 8 Zaidi ya hilo, Yehova Mungu akapanda bustani kule Edeni,+ kuelekea mashariki; na humo akamweka huyo mtu aliyemuumba.+ 9 Kwa hiyo Yehova Mungu akachipusha ardhini kila mti wenye kupendeza macho na unaofaa kwa chakula na pia mti wa uzima+ katikati ya bustani na mti wa ujuzi wa mema na mabaya.+

10 Sasa kulikuwa na mto uliotiririka kutoka Edeni ili kuinywesha bustani, na kutoka huko uligawanyika na kuwa mito minne.* 11 Jina la mto wa kwanza ni Pishoni; ndio unaozunguka nchi yote ya Havila, ambako kuna dhahabu. 12 Dhahabu ya nchi hiyo ni nzuri. Pia kuna utomvu wa mbedola na madini ya shohamu. 13 Jina la mto wa pili ni Gihoni; ndio unaozunguka nchi yote ya Kushi. 14 Jina la mto wa tatu ni Hidekeli;*+ ndio unaoelekea upande wa mashariki wa Ashuru.+ Na mto wa nne ni Efrati.+

15 Yehova Mungu akamchukua huyo mtu na kumweka katika bustani ya Edeni ili ailime na kuitunza.+ 16 Pia, Yehova Mungu akampa huyo mtu amri hii: “Unaweza kula matunda ya kila mti katika bustani mpaka ushibe.+ 17 Lakini kuhusu mti wa ujuzi wa mema na mabaya, usile matunda yake, kwa maana siku utakapokula matunda yake hakika utakufa.”+

18 Kisha Yehova Mungu akasema: “Si vema mwanamume huyu aendelee kuwa peke yake. Nitamuumbia msaidizi, awe kikamilisho chake.”+ 19 Sasa Yehova Mungu aliumba kutoka mavumbini kila mnyama wa mwituni na kila kiumbe anayeruka angani, naye akaanza kuwaleta kwa mtu huyo ili aamue jina atakalompa kila kiumbe; na jina lolote ambalo mtu huyo alimpa kila kiumbe aliye hai, likawa jina lake.+ 20 Basi mtu huyo akawapa majina wanyama wote wa kufugwa na viumbe wote wanaoruka angani na kila mnyama wa mwituni, lakini mwanamume huyo hakuwa na msaidizi ambaye angekuwa kikamilisho chake. 21 Kwa hiyo Yehova Mungu akamletea mwanamume huyo usingizi mzito, na alipokuwa akilala, akachukua ubavu wake mmoja na kufunika nyama mahali hapo. 22 Na Yehova Mungu akaufanya ubavu aliochukua kutoka kwa mwanamume uwe mwanamke, naye akamleta kwa mwanamume huyo.+

23 Ndipo mwanamume huyo akasema:

“Hatimaye huyu ni mfupa wa mifupa yangu

Na nyama ya nyama yangu.

Huyu ataitwa Mwanamke,

Kwa sababu alitolewa+ katika mwanamume.”

24 Ndiyo sababu mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana* na mke wake, nao watakuwa mwili mmoja.+ 25 Na wote wawili wakaendelea kuwa uchi,+ huyo mwanamume na mke wake; lakini hawakuona aibu.

3 Basi nyoka+ alikuwa mwenye kujihadhari* kuliko wanyama wote wa mwituni walioumbwa na Yehova Mungu. Kwa hiyo, akamuuliza mwanamke: “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?”+ 2 Mwanamke akamjibu nyoka: “Tunaweza kula matunda ya miti ya bustani.+ 3 Lakini Mungu amesema hivi kuhusu matunda ya mti ulio katikati ya bustani:+ ‘Msiyale, wala msiyaguse; la sivyo mtakufa.’” 4 Ndipo nyoka akamwambia mwanamke: “Hakika hamtakufa.+ 5 Kwa maana Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda ya mti huo, macho yenu yatafunguliwa nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”+

6 Kwa hiyo, mwanamke akaona kwamba mti huo ulifaa kwa chakula na kwamba ulikuwa kitu kinachotamanika kwa macho, naam, mti huo ulipendeza macho. Basi akaanza kuchuma matunda ya mti huo na kula.+ Baadaye, akampa pia mume wake baadhi ya matunda hayo alipokuwa pamoja naye, naye akaanza kula.+ 7 Ndipo macho yao wote wawili yakafunguliwa, nao wakatambua kwamba walikuwa uchi. Kwa hiyo wakayafunga pamoja majani ya mtini na kujitengenezea mavazi ya kujifunika kiunoni.+

8 Baadaye wakasikia sauti ya Yehova Mungu alipokuwa akitembea katika bustani wakati ambapo kuna upepo mtulivu, na mwanamume huyo na mke wake wakajificha katikati ya miti ya bustani kutoka mbele za uso wa Yehova Mungu. 9 Na Yehova Mungu akamwita huyo mwanamume tena na tena na kumuuliza: “Uko wapi?” 10 Mwishowe akajibu: “Niliisikia sauti yako katika bustani, lakini niliogopa kwa sababu nilikuwa uchi, basi nikajificha.” 11 Ndipo Mungu akamuuliza: “Ni nani aliyekwambia uko uchi?+ Je, umekula matunda ya mti niliokuamuru usile?”+ 12 Mwanamume huyo akasema: “Mwanamke uliyenipa nikae naye, alinipa tunda kutoka katika mti huo, basi nikala.” 13 Ndipo Yehova Mungu akamuuliza mwanamke: “Ni jambo gani hili ulilofanya?” Mwanamke akajibu: “Nyoka alinidanganya, basi nikala.”+

14 Kisha Yehova Mungu akamwambia nyoka:+ “Kwa sababu umefanya jambo hili, wewe umelaaniwa kati ya wanyama wote wa kufugwa na kati ya wanyama wote wa mwituni. Utakwenda kwa tumbo lako, nawe utakula mavumbi sikuzote za maisha yako. 15 Nami nitaweka uadui*+ kati yako+ na mwanamke+ na kati ya uzao wako*+ na uzao wake.*+ Yeye atakuponda* kichwa,+ nawe utamuuma* kisigino.”+

16 Akamwambia mwanamke: “Nitazidisha sana uchungu wa mimba yako; utazaa watoto kwa uchungu, nawe utamtamani sana mume wako, naye atakutawala.”

17 Kisha akamwambia Adamu:* “Kwa sababu uliisikiliza sauti ya mke wako na kula matunda ya mti ambao nilikuamuru+ hivi kuuhusu, ‘Usile matunda yake,’ ardhi imelaaniwa kwa sababu yako.+ Kwa maumivu utakula mazao yake sikuzote za maisha yako.+ 18 Itakuzalia miiba na michongoma, nawe utakula mimea ya shambani. 19 Kwa jasho la uso wako utakula chakula* mpaka utakaporudi ardhini, kwa kuwa ulitolewa humo.+ Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.”+

20 Baada ya hayo Adamu akampa mke wake jina Hawa,* kwa sababu angekuwa mama ya kila mtu anayeishi.+ 21 Na Yehova Mungu akamtengenezea Adamu na mke wake mavazi marefu ya ngozi ili wavae.+ 22 Kisha Yehova Mungu akasema: “Tazama mtu huyu amekuwa kama sisi kwa kujua mema na mabaya.+ Sasa ili asiunyooshe mkono wake na kuchukua pia matunda kutoka katika mti wa uzima,+ naye ale na kuishi milele,—” 23 Ndipo Yehova Mungu akamfukuza kutoka katika bustani ya Edeni+ ili ailime ardhi ambamo alikuwa ametolewa.+ 24 Basi akamfukuza mtu huyo, akaweka upande wa mashariki wa bustani ya Edeni makerubi+ na upanga unaowaka uliokuwa ukizunguka mfululizo ili kuilinda njia ya kwenda kwenye mti wa uzima.

4 Basi Adamu akafanya ngono na Hawa mke wake, na Hawa akapata mimba.+ Akamzaa Kaini+ na kusema: “Nimezaa mtoto wa kiume kwa msaada wa Yehova.” 2 Baadaye akamzaa Abeli,+ ndugu ya Kaini.

Abeli akawa mchungaji, lakini Kaini akawa mkulima. 3 Baada ya muda, Kaini alileta baadhi ya mazao ya shambani ili ayatoe kuwa dhabihu kwa Yehova. 4 Lakini Abeli alileta baadhi ya wazaliwa wa kwanza wa mifugo+ yake, pamoja na mafuta yao. Yehova alipendezwa na Abeli na dhabihu+ yake, 5 lakini hakupendezwa hata kidogo na Kaini na dhabihu yake. Basi Kaini akawaka hasira kali na kusononeka.* 6 Basi Yehova akamuuliza Kaini: “Kwa nini umekasirika sana na kusononeka? 7 Ukitenda mema, je, hutapata kibali tena?* Lakini usipotenda mema, dhambi inakunyemelea mlangoni, nayo inatamani sana kukutawala; lakini je, utaishinda?”

8 Baada ya hayo Kaini akamwambia Abeli ndugu yake: “Twende zetu shambani.” Basi walipokuwa shambani, Kaini akamshambulia Abeli ndugu yake, akamuua.+ 9 Baadaye, Yehova akamuuliza Kaini: “Yuko wapi Abeli ndugu yako?” naye akajibu: “Sijui. Kwani mimi ni mlinzi wa ndugu yangu?” 10 Basi Mungu akasema: “Umefanya nini? Sikiliza! Damu ya ndugu yako inanililia kwa sauti kutoka ardhini.+ 11 Na sasa umelaaniwa kwa kufukuzwa kutoka katika ardhi ambayo imefungua kinywa chake ili kupokea damu ya ndugu yako kutoka mkononi mwako.+ 12 Utakapolima ardhi, haitakurudishia mazao yake.* Utakuwa mtu anayetangatanga na mkimbizi duniani.” 13 Kisha Kaini akamwambia Yehova: “Adhabu ya kosa langu ni kubwa mno kwangu kustahimili. 14 Leo unanifukuza kutoka katika nchi hii,* nami nitafichwa kutoka mbele za uso wako; nitakuwa mtu anayetangatanga na mkimbizi duniani, na yeyote atakayenipata kwa hakika ataniua.” 15 Kwa hiyo Yehova akamwambia: “Kwa sababu hiyo, yeyote atakayemuua Kaini atalipizwa kisasi mara saba.”

Basi Yehova akaweka alama kwa ajili ya Kaini ili yeyote atakayempata asimuue. 16 Kisha Kaini akaenda zake kutoka mbele za Yehova, akaanza kuishi katika nchi ya Uhamisho,* upande wa mashariki wa Edeni.+

17 Baadaye Kaini akafanya ngono na mke wake,+ naye akapata mimba na kumzaa Enoko. Kisha akajenga jiji na kuliita jiji hilo Enoko, jina la mwanawe. 18 Baadaye Enoko akamzaa Iradi. Na Iradi akamzaa Mehuyaeli, na Mehuyaeli akamzaa Methushaeli, na Methushaeli akamzaa Lameki.

19 Lameki akaoa wake wawili. Mke wa kwanza aliitwa Ada, na wa pili aliitwa Zila. 20 Ada akamzaa Yabali. Ndiye aliyekuwa mwanzilishi wa wale wanaokaa katika mahema na wenye mifugo. 21 Ndugu yake aliitwa Yubali. Ndiye aliyekuwa mwanzilishi wa wale wote wanaopiga kinubi na zumari.* 22 Pia Zila alimzaa Tubal-kaini, aliyekuwa akitengeneza vifaa vya kila aina vya shaba na chuma. Na dada ya Tubal-kaini aliitwa Naama. 23 Kisha Lameki akatunga maneno haya kwa ajili ya wake zake, Ada na Zila:

“Sikieni sauti yangu, enyi wake za Lameki;

Sikilizeni maneno yangu:

Nimemuua mwanamume kwa sababu ya kunijeruhi,

Naam, mwanamume kijana kwa sababu ya kunipiga.

24 Ikiwa Kaini atalipizwa kisasi mara 7,+

Basi Lameki ni mara 77.”

25 Adamu akafanya ngono tena na mke wake, naye akazaa mwana. Akampa jina Sethi,*+ kwa sababu kama mama yake alivyosema, “Mungu amenichagulia mzao mwingine* atakayechukua mahali pa Abeli, kwa sababu Kaini alimuua.”+ 26 Pia Sethi akazaa mwana na kumpa jina Enoshi.+ Wakati huo watu walianza kuliitia jina la Yehova.

5 Hiki ndicho kitabu cha historia ya Adamu. Siku ambayo Mungu alimuumba Adamu, alimuumba kwa mfano wa Mungu.+ 2 Mwanamume na mwanamke aliwaumba.+ Siku ambayo aliwaumba,+ aliwabariki na kuwaita Binadamu.*

3 Adamu aliishi miaka 130, kisha akazaa mwana kwa mfano wake, kwa sura yake, akampa jina Sethi.+ 4 Baada ya kumzaa Sethi, Adamu aliishi miaka 800. Naye akazaa wana na mabinti. 5 Basi siku zote za maisha ya Adamu zilikuwa miaka 930, kisha akafa.+

6 Sethi aliishi miaka 105, akamzaa Enoshi.+ 7 Baada ya kumzaa Enoshi, Sethi aliishi miaka 807. Naye akazaa wana na mabinti. 8 Basi siku zote za maisha ya Sethi zilikuwa miaka 912, kisha akafa.

9 Enoshi aliishi miaka 90, kisha akamzaa Kenani. 10 Baada ya kumzaa Kenani, Enoshi aliishi miaka 815. Naye akazaa wana na mabinti. 11 Basi siku zote za maisha ya Enoshi zilikuwa miaka 905, kisha akafa.

12 Kenani aliishi miaka 70, kisha akamzaa Mahalaleli.+ 13 Baada ya kumzaa Mahalaleli, Kenani aliishi miaka 840. Naye akazaa wana na mabinti. 14 Basi siku zote za maisha ya Kenani zilikuwa miaka 910, kisha akafa.

15 Mahalaleli aliishi miaka 65, kisha akamzaa Yaredi.+ 16 Baada ya kumzaa Yaredi, Mahalaleli aliishi miaka 830. Naye akazaa wana na mabinti. 17 Basi siku zote za maisha ya Mahalaleli zilikuwa miaka 895, kisha akafa.

18 Yaredi aliishi miaka 162, kisha akamzaa Enoko.+ 19 Baada ya kumzaa Enoko, Yaredi aliishi miaka 800. Naye akazaa wana na mabinti. 20 Basi siku zote za maisha ya Yaredi zilikuwa miaka 962, kisha akafa.

21 Enoko aliishi miaka 65, kisha akamzaa Methusela.+ 22 Baada ya kumzaa Methusela, Enoko aliendelea kutembea na Mungu wa kweli kwa miaka 300. Naye akazaa wana na mabinti. 23 Basi siku zote za maisha ya Enoko zilikuwa miaka 365. 24 Enoko aliendelea kutembea na Mungu wa kweli.+ Kisha hakuwepo tena, kwa maana Mungu alimchukua.+

25 Methusela aliishi miaka 187, kisha akamzaa Lameki.+ 26 Baada ya kumzaa Lameki, Methusela aliishi miaka 782. Naye akazaa wana na mabinti. 27 Basi siku zote za maisha ya Methusela zilikuwa miaka 969, kisha akafa.

28 Lameki aliishi miaka 182, kisha akazaa mwana. 29 Akamwita mwana huyo Noa,*+ akisema: “Huyu atatufariji katika kazi yetu ngumu na katika kazi inayoumiza ya mikono yetu kwa sababu ya ardhi iliyolaaniwa+ na Yehova.” 30 Baada ya kumzaa Noa, Lameki aliishi miaka 595. Naye akazaa wana na mabinti. 31 Basi siku zote za maisha ya Lameki zilikuwa miaka 777, kisha akafa.

32 Baada ya Noa kuishi miaka 500, alimzaa Shemu,+ Hamu,+ na Yafethi.+

6 Sasa idadi ya wanadamu ilipoanza kuongezeka duniani, nao wakazaa mabinti, 2 wana wa Mungu wa kweli*+ wakaanza kuona kwamba mabinti wa wanadamu ni warembo. Basi wakaanza kuwachukua wote waliowachagua ili wawe wake zao. 3 Ndipo Yehova akasema: “Roho yangu haitamvumilia mwanadamu daima,+ kwa sababu yeye ni mwili tu.* Kwa hiyo, jumla ya siku zake itakuwa miaka 120.”+

4 Wanefili* walikuwa duniani siku hizo na baadaye. Wakati huo wana wa Mungu wa kweli waliendelea kufanya ngono na mabinti wa wanadamu, nao wakawazalia wana. Wana hao walikuwa watu wenye nguvu wa nyakati za kale, wanaume maarufu.

5 Basi, Yehova akaona kwamba uovu wa mwanadamu ulikuwa mkubwa duniani na kwamba kila mwelekeo wa mawazo ya moyo wake ulikuwa mbaya tu wakati wote.+ 6 Yehova akaghairi* kwamba aliwaumba wanadamu duniani, na moyo wake ukahuzunika.*+ 7 Kwa hiyo Yehova akasema: “Nitawafagilia mbali kutoka duniani wanadamu ambao nimewaumba, wanadamu pamoja na wanyama wa kufugwa, wanyama wanaotambaa, na viumbe wanaoruka angani, kwa sababu ninaghairi kwamba niliwaumba.” 8 Lakini Noa akapata kibali machoni pa Yehova.

9 Hii ndiyo historia ya Noa.

Noa alikuwa mtu mwadilifu.+ Alijithibitisha mwenyewe kuwa mtu asiye na kosa* miongoni mwa watu wa siku zake.* Noa alitembea pamoja na Mungu wa kweli.+ 10 Baada ya muda, Noa alizaa wana watatu, Shemu, Hamu, na Yafethi.+ 11 Lakini dunia ilikuwa imeharibika machoni pa Mungu wa kweli, nayo dunia ilikuwa imejaa ukatili. 12 Naam, Mungu aliitazama dunia, nayo ilikuwa imeharibika;+ watu wote walikuwa wameharibu njia yao duniani.+

13 Baada ya hayo Mungu akamwambia Noa: “Nimeamua kuwaangamiza wanadamu wote, kwa sababu wameijaza dunia ukatili, kwa hiyo nitawaangamiza pamoja na dunia.+ 14 Jitengenezee safina* kwa mbao za mti wenye utomvu.+ Utatengeneza vyumba ndani ya safina na uifunike kwa lami+ ndani na nje. 15 Hivi ndivyo utakavyoitengeneza: Safina inapaswa kuwa na urefu wa mikono 300,* upana wa mikono 50, na kimo cha mikono 30. 16 Utatengeneza dirisha la kuingiza mwangaza kwenye safina,* mkono mmoja kutoka juu. Unapaswa kutengeneza mlango ubavuni mwake,+ na utengeneze ghorofa ya chini, ghorofa ya pili, na ghorofa ya tatu.

17 “Nami kwa upande wangu, nitaleta gharika ya maji+ duniani ili kuangamiza viumbe wote wenye pumzi ya uhai* walio chini ya mbingu. Kila kitu kilicho duniani kitaangamia.+ 18 Nami ninafanya pamoja nawe agano langu, nawe lazima uingie ndani ya safina, wewe, wanao, mke wako, na wake wa wanao.+ 19 Nawe uingize ndani ya safina viumbe hai+ wawili wawili wa kila aina ili kuwahifadhi hai pamoja nawe, dume na jike;+ 20 viumbe wanaoruka angani kulingana na aina zao, wanyama wa kufugwa kulingana na aina zao, na wanyama wote wanaotambaa kulingana na aina zao, watakuja ndani kwako viumbe wawili wawili wa kila aina ili uwahifadhi hai.+ 21 Nawe unapaswa kukusanya na kuchukua kila aina ya chakula,+ kwa ajili yako na wanyama.”

22 Basi Noa akafanya kulingana na mambo yote ambayo Mungu alikuwa amemwamuru. Hivyo ndivyo alivyofanya.+

7 Baada ya hayo Yehova akamwambia Noa: “Ingia ndani ya safina, wewe pamoja na watu wote wa nyumbani mwako, kwa sababu nimekuona wewe peke yako kuwa mwadilifu mbele zangu miongoni mwa kizazi hiki.+ 2 Ingia pamoja na wanyama safi wa kila aina, saba saba,*+ dume na jike; na wanyama wawili tu wasio safi wa kila aina, dume na jike; 3 pia viumbe wanaoruka angani saba saba,* dume na jike, ili kuhifadhi hai uzao wao duniani pote.+ 4 Kwa maana baada ya siku saba tu, nitafanya mvua inyeshe+ duniani siku 40 mchana na usiku,+ nami nitafagilia mbali kutoka duniani kila kiumbe kilicho hai nilichokiumba.”+ 5 Basi Noa akafanya yote ambayo Yehova alikuwa amemwamuru.

6 Noa alikuwa na umri wa miaka 600 maji ya gharika yalipokuja duniani.+ 7 Kwa hiyo Noa, pamoja na wanawe, mke wake, na wake wa wanawe, wakaingia ndani ya safina kabla ya maji ya gharika kuja.+ 8 Kila aina ya mnyama aliye safi na kila aina ya mnyama asiye safi na kila aina ya kiumbe anayeruka angani na kila aina ya kiumbe anayetambaa ardhini,+ 9 wakaingia wawili wawili na kumjia Noa ndani ya safina, dume na jike, kama Mungu alivyokuwa amemwamuru Noa. 10 Na siku saba baadaye maji ya gharika yakaja duniani.

11 Katika mwaka wa 600 wa maisha ya Noa, mwezi wa pili, siku ya 17 ya mwezi huo, siku hiyo chemchemi zote za kilindi kikubwa cha maji zilifunguka kwa nguvu na malango ya mbinguni ya mafuriko yakafunguliwa.+ 12 Na mvua ikamwagika duniani kwa siku 40, mchana na usiku. 13 Siku hiyohiyo, Noa aliingia ndani ya safina pamoja na wanawe, Shemu, Hamu, na Yafethi,+ pamoja na mke wake na wake watatu wa wanawe.+ 14 Waliingia ndani pamoja na kila mnyama wa mwituni kulingana na aina yake, na kila mnyama wa kufugwa kulingana na aina yake, na kila mnyama anayetambaa duniani kulingana na aina yake, na kila kiumbe anayeruka kulingana na aina yake, kila ndege, kila kiumbe mwenye mabawa. 15 Waliendelea kumjia Noa ndani ya safina, wawili wawili, kila aina ya kiumbe mwenye pumzi ya uhai.* 16 Basi wakaingia ndani, dume na jike, viumbe wa kila aina, kama Mungu alivyokuwa amemwamuru. Baada ya hayo Yehova akaufunga mlango.

17 Gharika ikaendelea* kwa siku 40 duniani, na maji yakazidi kuongezeka, yakaanza kuibeba safina, nayo safina ikaelea juu sana duniani. 18 Maji yakafurika na kuzidi kuongezeka sana duniani, lakini safina ilielea juu ya maji. 19 Maji yalifurika sana duniani hivi kwamba milima yote mirefu chini ya mbingu ikafunikwa.+ 20 Maji yalipanda kufikia mikono 15* juu ya milima.

21 Basi viumbe wote walio hai waliotembea duniani wakafa+—viumbe wanaoruka, wanyama wa kufugwa, wanyama wa mwituni, viumbe wanaoishi katika makundi makubwa, na wanadamu wote.+ 22 Kila kiumbe katika nchi kavu aliyekuwa na pumzi ya uhai* katika mianzi ya pua yake akafa.+ 23 Basi Mungu akafagilia mbali kila kiumbe hai kutoka duniani, kutia ndani, wanadamu, wanyama, wanyama wanaotambaa, na viumbe wanaoruka angani. Wote walifagiliwa mbali kutoka duniani;+ ni Noa peke yake na wale waliokuwa pamoja naye ndani ya safina waliookoka.+ 24 Na maji yakaendelea kuifunika dunia kwa siku 150.+

8 Lakini Mungu akamwelekezea uangalifu* Noa na wanyama wote wa mwituni na wanyama wa kufugwa waliokuwa pamoja naye ndani ya safina,+ na Mungu akavumisha upepo duniani, maji yakaanza kupungua. 2 Chemchemi za kilindi cha maji na malango ya mbinguni ya mafuriko yakafungwa, kwa hiyo mvua kutoka mbinguni ikaacha kunyesha.*+ 3 Kisha maji yakaanza kupungua hatua kwa hatua duniani. Kufikia mwishoni mwa siku 150, maji yalikuwa yamepungua sana. 4 Katika mwezi wa saba, siku ya 17 ya mwezi huo, safina ikatua kwenye milima ya Ararati. 5 Na maji yakazidi kupungua hatua kwa hatua mpaka mwezi wa kumi. Katika mwezi wa kumi, siku ya kwanza ya mwezi huo, vilele vya milima vikaonekana.+

6 Basi mwishoni mwa siku 40, Noa akafungua dirisha+ la safina alilokuwa ametengeneza 7 na kumtuma nje kunguru; kunguru alikuwa akienda na kurudi, mpaka maji yalipokauka duniani.

8 Baadaye akamtuma njiwa ili aone ikiwa maji yalikuwa yamepungua ardhini. 9 Njiwa huyo hakupata mahali pa kutua,* kwa hiyo akarudi kwa Noa ndani ya safina kwa sababu maji yalikuwa bado yameifunika dunia yote.+ Kwa hiyo akaunyoosha mkono wake nje na kumwingiza ndani ya safina. 10 Noa akangojea siku saba zaidi, akamtuma tena njiwa nje ya safina. 11 Njiwa huyo alipomrudia Noa ikielekea jioni, aliona kwamba alikuwa na jani bichi la mzeituni mdomoni mwake! Basi Noa akajua kwamba maji yalikuwa yamepungua duniani.+ 12 Akangojea tena siku nyingine saba. Kisha akamtuma nje njiwa huyo, lakini hakurudi tena.

13 Sasa katika mwaka wa 601,+ mwezi wa kwanza, siku ya kwanza ya mwezi huo, maji yalikuwa yamepungua duniani; Noa akaondoa kifuniko cha safina na kuona kwamba ardhi ilikuwa ikikauka. 14 Katika mwezi wa pili, siku ya 27 ya mwezi huo, dunia ilikuwa imekauka.

15 Sasa Mungu akamwambia Noa: 16 “Toka ndani ya safina, wewe, mke wako, wanao, na wake zao.+ 17 Toka pamoja na viumbe wote walio hai wa kila aina,+ viumbe wanaoruka, wanyama, na wanyama wote wanaotambaa, ili wazaane* duniani na kuongezeka na kuwa wengi duniani.”+

18 Basi Noa akatoka nje, pamoja na wanawe,+ mke wake, na wake wa wanawe. 19 Kila kiumbe aliye hai, kila mnyama anayetambaa na kila kiumbe anayeruka, kila kiumbe anayetembea duniani, akatoka ndani ya safina kulingana na familia yake.+ 20 Kisha Noa akamjengea Yehova madhabahu,+ akachukua baadhi ya wanyama walio safi na baadhi ya viumbe wanaoruka walio safi,+ akawatoa kuwa dhabihu za kuteketezwa juu ya madhabahu+ hiyo. 21 Na Yehova akaanza kusikia harufu ya kupendeza.* Kwa hiyo Yehova akasema moyoni mwake: “Sitailaani ardhi+ tena kwa sababu ya mwanadamu, kwa maana mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu wakati wa ujana;+ nami sitamwangamiza tena kamwe kila kiumbe aliye hai kama nilivyofanya.+ 22 Kuanzia sasa na kuendelea, dunia haitakosa kamwe kuwa na majira ya kupanda mbegu na kuvuna, baridi na joto, kiangazi na masika, na mchana na usiku.”+

9 Basi Mungu akambariki Noa na wanawe na kuwaambia: “Zaeni muwe wengi na kuijaza dunia.+ 2 Kila kiumbe aliye hai duniani na kila kiumbe anayeruka angani na kila kiumbe anayetambaa ardhini na samaki wote wa baharini wataendelea kuwaogopa na kuwahofu ninyi. Sasa nimewatia mikononi mwenu.*+ 3 Kila mnyama aliye hai anayetembea anaweza kuwa chakula chenu.+ Kama nilivyowapa mimea, ninawapa hao wote wawe chakula chenu.+ 4 Ila tu nyama pamoja na uhai wake*—damu yake+—hampaswi kula.+ 5 Zaidi ya hayo, nitadai muwajibike kwa sababu ya damu ya uhai wenu.* Nitadai kila kiumbe aliye hai awajibike; nami nitamdai kila mwanadamu awajibike kwa sababu ya uhai wa ndugu yake.+ 6 Yeyote anayemwaga damu ya mwanadamu, damu yake mwenyewe itamwagwa+ na mwanadamu, kwa maana Mungu alimuumba mwanadamu+ kwa mfano Wake. 7 Lakini ninyi, zaeni muwe wengi, mwongezeke kwa wingi na kujaa+ duniani.”

8 Kisha Mungu akamwambia Noa na wanawe: 9 “Sasa ninafanya agano langu pamoja nanyi+ na pamoja na wazao wenu baada yenu, 10 na pamoja na kila kiumbe aliye hai ambaye yupo* pamoja nanyi, ndege, wanyama, na viumbe wote walio hai duniani pamoja nanyi, wote waliotoka ndani ya safina—kila kiumbe aliye hai duniani.+ 11 Naam, ninafanya agano langu pamoja nanyi: Viumbe wote* hawataangamizwa tena kamwe kwa maji ya gharika, na gharika haitaiharibu+ dunia tena kamwe.”

12 Na Mungu akaendelea kusema: “Hii ndiyo ishara ya agano ninalofanya pamoja nanyi na pamoja na kila kiumbe hai aliye pamoja nanyi, kwa vizazi vyote vijavyo. 13 Ninauweka upinde wangu wa mvua mawinguni, nao utakuwa ishara ya agano nililofanya na dunia. 14 Kila mara ninapoleta mawingu juu ya dunia, kwa hakika upinde wa mvua utaonekana mawinguni. 15 Nami hakika nitakumbuka agano langu nililofanya pamoja nanyi na pamoja na kila aina ya kiumbe aliye hai; na kamwe hakutakuwa tena na gharika ya maji itakayowaangamiza viumbe wote.+ 16 Na upinde wa mvua utatokea mawinguni, nami hakika nitauona na kukumbuka agano la milele ambalo mimi Mungu nilifanya pamoja na kila aina ya kiumbe hai duniani.”

17 Mungu akarudia kumwambia Noa: “Hii ndiyo ishara ya agano ninalofanya pamoja na viumbe wote walio duniani.”+

18 Hawa ndio wana wa Noa waliotoka ndani ya safina: Shemu, Hamu, na Yafethi.+ Baadaye Hamu akamzaa Kanaani.+ 19 Hao watatu walikuwa wana wa Noa, na watu wote duniani walitokana nao na kuenea kotekote.+

20 Sasa Noa akaanza kulima, akapanda shamba la mizabibu. 21 Alipokunywa divai, alilewa, naye akavua nguo ndani ya hema lake. 22 Hamu, baba ya Kanaani, akamwona baba yake akiwa uchi, akawaambia ndugu zake wawili waliokuwa nje. 23 Kwa hiyo Shemu na Yafethi wakachukua nguo na kuiweka mabegani mwao na kuingia ndani kinyumenyume. Basi wakaufunika uchi wa baba yao huku nyuso zao zikitazama pembeni, nao hawakuuona uchi wa baba yao.

24 Divai ilipomtoka Noa, naye akasikia jambo ambalo mwanawe mdogo alimtendea, 25 akasema:

“Alaaniwe Kanaani.+

Na awe mtumwa wa hali ya chini kabisa kwa ndugu zake.”+

26 Pia akasema:

“Asifiwe Yehova, Mungu wa Shemu,

Acha Kanaani awe mtumwa wake.+

27 Mungu na ampe Yafethi nafasi ya kutosha,

Na akae katika mahema ya Shemu.

Kanaani na awe mtumwa wake pia.”

28 Noa akaendelea kuishi miaka 350 baada ya Gharika.+ 29 Basi siku zote za maisha ya Noa zilikuwa miaka 950, kisha akafa.

10 Hii ndiyo historia ya wana wa Noa, yaani, Shemu,+ Hamu, na Yafethi.

Walizaa wana baada ya Gharika.+ 2 Wana wa Yafethi walikuwa Gomeri,+ Magogu,+ Madai, Yavani, Tubali,+ Mesheki,+ na Tirasi.+

3 Wana wa Gomeri walikuwa Ashkenazi,+ Rifathi, na Togarma.+

4 Wana wa Yavani walikuwa Elisha,+ Tarshishi,+ Kitimu,+ na Dodanimu.

5 Kutokana na hawa, wakaaji wa visiwani walienea katika nchi zao, kulingana na lugha zao na koo zao na kulingana na mataifa yao.

6 Wana wa Hamu walikuwa Kushi, Misraimu,+ Putu,+ na Kanaani.+

7 Wana wa Kushi walikuwa Seba,+ Havila, Sabta, Raama,+ na Sabteka.

Wana wa Raama walikuwa Sheba na Dedani.

8 Kushi akamzaa Nimrodi. Nimrodi ndiye aliyekuwa shujaa wa kwanza duniani. 9 Alikuwa mwindaji hodari aliyempinga Yehova. Ndiyo sababu kuna msemo usemao: “Kama Nimrodi, mwindaji hodari aliyempinga Yehova.” 10 Ufalme wake ulianzia* Babeli,+ Ereki,+ Akadi, na Kalne, katika nchi ya Shinari.+ 11 Kutoka katika nchi hiyo alienda Ashuru+ na kujenga Ninawi,+ Rehoboth-Iri, Kala, 12 na Reseni, kati ya Ninawi na Kala: Hilo ndilo lile jiji kubwa.*

13 Misraimu akamzaa Ludimu,+ Anamimu, Lehabimu, Naftuhimu,+ 14 Pathrusimu,+ Kasluhimu (hao ndio waliowazaa Wafilisti),+ na Kaftorimu.+

15 Kanaani akamzaa Sidoni,+ mzaliwa wake wa kwanza, na Hethi,+ 16 na pia Wayebusi,+ Waamori,+ Wagirgashi, 17 Wahivi,+ Waarkia, Wasini, 18 Waarvadi,+ Wasemari, na Wahamathi.+ Baadaye, koo za Wakanaani zilitawanyika. 19 Basi mpaka wa Wakanaani ulianzia Sidoni mpaka Gerari,+ karibu na Gaza,+ hadi Sodoma, Gomora,+ Adma, na Seboiimu,+ karibu na Lasha. 20 Hao ndio waliokuwa wana wa Hamu kulingana na koo zao, lugha zao, nchi zao, na mataifa yao.

21 Shemu, babu ya wana wote wa Eberi+ na ndugu ya Yafethi mkubwa kuliko wote,* pia alizaa watoto. 22 Wana wa Shemu walikuwa Elamu,+ Asihuru,+ Arpakshadi,+ Ludi, na Aramu.+

23 Wana wa Aramu walikuwa Usi, Huli, Getheri, na Mashi.

24 Arpakshadi akamzaa Shela,+ naye Shela akamzaa Eberi.

25 Eberi alizaa wana wawili. Mmoja aliitwa Pelegi,*+ kwa sababu katika siku zake dunia ilikuwa imegawanyika.* Ndugu yake aliitwa Yoktani.+

26 Yoktani akamzaa Almodadi, Shelefu, Hazarmavethi, Yera,+ 27 Hadoramu, Uzali, Dikla, 28 Obali, Abimaeli, Sheba, 29 Ofiri,+ Havila, na Yobabu; wote hao walikuwa wana wa Yoktani.

30 Nchi walimokaa ilianzia Mesha mpaka Sefari, eneo lenye milima la Mashariki.

31 Hao ndio waliokuwa wana wa Shemu kulingana na koo zao, lugha zao, nchi zao, na mataifa yao.+

32 Hizo ndizo zilizokuwa familia za wana wa Noa kulingana na koo zao na mataifa yao. Kutokana nao, mataifa yalienea duniani kote baada ya Gharika.+

11 Sasa dunia yote iliendelea kuwa na lugha moja na maneno yaleyale.* 2 Walipokuwa wakisafiri kuelekea mashariki, waligundua bonde tambarare katika nchi ya Shinari,+ wakaanza kuishi huko. 3 Kisha wakaambiana: “Njooni! Tufyatue matofali na kuyachoma.” Basi wakatumia matofali badala ya mawe, na lami badala ya saruji. 4 Sasa wakasema: “Haya! Na tujijengee jiji na mnara ambao kilele chake kitafika mbinguni, na tujijengee jina maarufu, ili tusitawanyike katika dunia yote.”+

5 Kisha Yehova akashuka ili aone jiji na mnara ambao wanadamu walikuwa wamejenga. 6 Ndipo Yehova akasema: “Tazama! Watu hawa ni kitu kimoja na wanazungumza lugha moja,+ na hili ndilo jambo waliloanza kufanya. Sasa hakuna jambo lolote wanalokusudia kufanya litakalowashinda. 7 Njooni! Tushuke+ huko na kuvuruga lugha yao ili kila mmoja wao asiielewe lugha ya mwenzake.” 8 Basi Yehova akawatawanya duniani pote+ kutoka huko, na hatua kwa hatua wakaacha kujenga jiji hilo. 9 Ndiyo sababu liliitwa Babeli,*+ kwa sababu huko ndiko Yehova alikovuruga lugha ya dunia yote, na kutoka huko Yehova aliwatawanya duniani pote.

10 Hii ndiyo historia ya Shemu.+

Shemu alikuwa na umri wa miaka 100 alipomzaa Arpakshadi+ miaka miwili baada ya Gharika. 11 Baada ya kumzaa Arpakshadi, Shemu aliishi miaka 500. Akazaa wana na mabinti.+

12 Arpakshadi alipokuwa na umri wa miaka 35, alimzaa Shela.+ 13 Baada ya kumzaa Shela, Arpakshadi aliishi miaka 403. Akazaa wana na mabinti.

14 Shela alipokuwa na umri wa miaka 30, alimzaa Eberi.+ 15 Baada ya kumzaa Eberi, Shela aliishi miaka 403. Akazaa wana na mabinti.

16 Eberi alipokuwa na umri wa miaka 34, alimzaa Pelegi.+ 17 Baada ya kumzaa Pelegi, Eberi aliishi miaka 430. Akazaa wana na mabinti.

18 Pelegi alipokuwa na umri wa miaka 30, alimzaa Reu.+ 19 Baada ya kumzaa Reu, Pelegi aliishi miaka 209. Akazaa wana na mabinti.

20 Reu alipokuwa na umri wa miaka 32, alimzaa Serugi. 21 Baada ya kumzaa Serugi, Reu aliishi miaka 207. Akazaa wana na mabinti.

22 Serugi alipokuwa na umri wa miaka 30, alimzaa Nahori. 23 Baada ya kumzaa Nahori, Serugi aliishi miaka 200. Akazaa wana na mabinti.

24 Nahori alipokuwa na umri wa miaka 29, alimzaa Tera.+ 25 Baada ya kumzaa Tera, Nahori aliishi miaka 119. Akazaa wana na mabinti.

26 Tera alipokuwa na umri wa miaka 70, alimzaa Abramu,+ Nahori,+ na Harani.

27 Hii ndiyo historia ya Tera.

Tera alimzaa Abramu, Nahori, na Harani; naye Harani akamzaa Loti.+ 28 Tera, baba yake, alipokuwa bado hai, Harani alikufa katika nchi alimozaliwa, katika jiji la Uru+ la Wakaldayo.+ 29 Abramu na Nahori wakapata wake. Mke wa Abramu aliitwa Sarai,+ na mke wa Nahori aliitwa Milka, binti ya Harani, baba ya Milka+ na Iska. 30 Sasa Sarai alikuwa tasa;+ hakuwa na mtoto.

31 Kisha Tera akamchukua Abramu mwanawe na Loti mjukuu wake,+ mwana wa Harani, na Sarai binti mkwe wake, mke wa Abramu mwanawe, wakaondoka pamoja naye katika jiji la Uru la Wakaldayo ili kwenda katika nchi ya Kanaani.+ Baada ya muda wakafika Harani+ na kuanza kukaa huko. 32 Tera aliishi miaka 205. Kisha Tera akafa huko Harani.

12 Yehova akamwambia Abramu: “Ondoka katika nchi yako na kutoka kwa watu wako wa ukoo na nyumba ya baba yako uende katika nchi nitakayokuonyesha;+ 2 Nitakufanya kuwa taifa kubwa, nami nitakubariki, nami nitalifanya jina lako liwe kuu, nawe utakuwa baraka.+ 3 Nitawabariki wale wanaokubariki, nami nitawalaani wale wanaokulaani,+ na familia zote duniani hakika zitabarikiwa* kupitia kwako.”+

4 Basi Abramu akaondoka kama Yehova alivyokuwa amemwambia, na Loti akaondoka pamoja naye. Abramu alikuwa na umri wa miaka 75 alipoondoka Harani.+ 5 Abramu akamchukua Sarai+ mke wake na Loti mwana wa ndugu yake+ na mali zote ambazo walikuwa wamekusanya+ na watu ambao walikuwa wamejipatia huko Harani, nao wakaanza safari ya kwenda katika nchi ya Kanaani.+ Walipofika nchi ya Kanaani, 6 Abramu akasafiri nchini mpaka eneo la Shekemu,+ karibu na miti mikubwa ya More.+ Wakati huo Wakanaani walikuwa katika nchi hiyo. 7 Kisha Yehova akamtokea Abramu na kumwambia: “Nitaupa uzao wako*+ nchi hii.”+ Basi akamjengea Yehova madhabahu huko, aliyekuwa amemtokea. 8 Baadaye akatoka huko na kwenda katika eneo lenye milima upande wa mashariki wa Betheli+ na kupiga hema lake, jiji la Betheli likiwa upande wa magharibi na Ai+ upande wa mashariki. Huko, akamjengea Yehova+ madhabahu na kuanza kuliitia jina la Yehova.+ 9 Baadaye, Abramu akavunja kambi na kusafiri kuelekea Negebu,+ akihamisha kambi yake kutoka sehemu moja hadi nyingine.

10 Sasa njaa kali ikatokea nchini, na Abramu akateremka kuelekea Misri ili akae huko kwa muda fulani,*+ kwa sababu njaa hiyo ilikuwa kali sana.+ 11 Alipokaribia kuingia Misri, akamwambia Sarai mke wake: “Tafadhali sikiliza! Ninajua kwamba wewe ni mwanamke mrembo sana.+ 12 Kwa hiyo Wamisri watakapokuona, hakika watasema, ‘Huyu ni mke wake.’ Halafu wataniua, lakini wewe watakuacha hai. 13 Tafadhali waambie wewe ni dada yangu, ili mambo yaniendee vema kwa sababu yako, nao hawataniua.”*+

14 Mara tu Abramu alipoingia Misri, Wamisri waliona kwamba mwanamke huyo alikuwa mrembo sana. 15 Na maofisa wa Farao walimwona pia, nao wakaanza kumsifu mbele ya Farao, kwa hiyo mwanamke huyo akapelekwa katika nyumba ya Farao. 16 Farao alimtendea Abramu vema kwa sababu ya Sarai, naye akapata kondoo, ng’ombe, punda madume na majike, watumishi wa kiume na wa kike, na ngamia.+ 17 Ndipo Yehova akampiga Farao na watu wa nyumbani mwake kwa mapigo makali kwa sababu ya Sarai, mke wa Abramu.+ 18 Basi Farao akamwita Abramu na kumuuliza: “Kwa nini umenitendea hivi? Kwa nini hukuniambia kwamba yeye ni mke wako? 19 Kwa nini ulisema, ‘Huyu ni dada yangu,’+ hivi kwamba nilikuwa karibu kumchukua awe mke wangu? Mke wako ndiye huyu. Mchukue uende zako!” 20 Kwa hiyo Farao akawapa maofisa wake maagizo kumhusu, nao wakamwacha aende zake pamoja na mke wake na vyote alivyokuwa navyo.+

13 Kisha Abramu akapanda kutoka Misri kwenda Negebu,+ yeye pamoja na mke wake na vitu vyote alivyokuwa navyo, pamoja na Loti. 2 Abramu alikuwa na utajiri mwingi wa mifugo, fedha, na dhahabu.+ 3 Alipiga kambi sehemu moja baada ya nyingine aliposafiri kutoka Negebu kwenda Betheli, mpaka alipofika mahali alipokuwa amepiga hema lake kati ya Betheli na Ai,+ 4 mahali alipokuwa amejenga madhabahu mwanzoni. Huko, Abramu akaliitia jina la Yehova.

5 Sasa Loti, aliyekuwa akisafiri pamoja na Abramu, alikuwa pia na kondoo, ng’ombe, na mahema. 6 Basi wote hawangeweza kukaa pamoja kwa sababu nchi haikuwatosha; mali zao zilikuwa zimeongezeka sana hivi kwamba hawangeweza tena kukaa pamoja. 7 Kwa sababu hiyo, ugomvi ukatokea kati ya wachungaji wa mifugo ya Abramu na wachungaji wa mifugo ya Loti. (Wakati huo Wakanaani na Waperizi walikuwa wakikaa katika nchi hiyo.)+ 8 Basi Abramu akamwambia Loti:+ “Tafadhali, pasiwe na ugomvi wowote kati yangu mimi na wewe na kati ya wachungaji wangu na wachungaji wako, kwa maana sisi ni ndugu. 9 Je, nchi yote haiko mbele yako? Tafadhali, jitenge nami. Ukienda kushoto, nitakwenda kulia; lakini ukienda kulia, basi mimi nitakwenda kushoto.” 10 Kwa hiyo Loti akainua macho yake na kuona kwamba wilaya yote ya Yordani+ ilikuwa na maji ya kutosha (kabla Yehova hajaharibu Sodoma na Gomora), kama bustani ya Yehova,+ kama nchi ya Misri, mpaka Soari.+ 11 Basi Loti akajichagulia wilaya yote ya Yordani, naye Loti akahamisha kambi yake kuelekea upande wa mashariki. Kwa hiyo wakatengana. 12 Abramu aliishi katika nchi ya Kanaani, lakini Loti aliishi katika majiji ya wilaya hiyo.+ Hatimaye akapiga hema lake karibu na Sodoma. 13 Sasa watu wa Sodoma walikuwa waovu, nao walitenda dhambi nzito machoni pa Yehova.+

14 Yehova akamwambia hivi Abramu baada ya Loti kujitenga naye: “Tafadhali, inua macho yako, na kutoka mahali ulipo tazama kaskazini na kusini, mashariki na magharibi, 15 kwa sababu nchi yote unayoona, nitakupa wewe na uzao wako* iwe miliki yenu ya kudumu.+ 16 Nami nitaufanya uzao wako uwe* kama chembe za mavumbi ya ardhi, hivi kwamba ikiwa kuna yeyote anayeweza kuhesabu chembe za mavumbi ya ardhi, basi uzao wako utaweza* kuhesabiwa.+ 17 Ondoka, safiri kwa mapana na marefu katika nchi hii, kwa maana nitakupa wewe nchi hii.” 18 Basi Abramu akaendelea kuishi katika mahema. Baadaye akaja na kuishi kati ya miti mikubwa ya Mamre,+ ambayo iko Hebroni,+ na huko akamjengea Yehova madhabahu.+

14 Sasa katika siku za Amrafeli mfalme wa Shinari,+ Arioko mfalme wa Elasari, Kedorlaoma+ mfalme wa Elamu,+ na Tidali mfalme wa Goiimu, 2 wafalme hawa walikwenda kupigana vita na Bera mfalme wa Sodoma,+ Birsha mfalme wa Gomora,+ Shinabu mfalme wa Adma, Shemeberi mfalme wa Seboiimu,+ na mfalme wa Bela, yaani, Soari. 3 Hao wote waliungana pamoja katika Bonde la* Sidimu,+ yaani, Bahari ya Chumvi.+

4 Walikuwa wamemtumikia Kedorlaoma kwa miaka 12, lakini wakaasi katika mwaka wa 13. 5 Kwa hiyo katika mwaka wa 14, Kedorlaoma na wafalme waliokuwa pamoja naye wakaja na kuwashinda Warefaimu waliokuwa Ashteroth-karnaimu, Wazuzi waliokuwa Hamu, Waemi+ waliokuwa Shave-kiriathaimu, 6 na Wahori+ katika mlima wao wa Seiri+ na kuteremka mpaka El-parani, eneo lililo nyikani. 7 Kisha wakarudi nyuma na kwenda En-mishpati, yaani, Kadeshi,+ wakashinda eneo lote la Waamaleki+ na pia Waamori+ waliokuwa wakiishi Hasason-tamari.+

8 Ndipo mfalme wa Sodoma akapiga mwendo, na pia mfalme wa Gomora, mfalme wa Adma, mfalme wa Seboiimu, na mfalme wa Bela, yaani, Soari, nao wakajipanga kivita ili kupigana nao katika Bonde la* Sidimu, 9 ili kupigana na Kedorlaoma mfalme wa Elamu, Tidali mfalme wa Goiimu, Amrafeli mfalme wa Shinari, na Arioko mfalme wa Elasari+—wafalme wanne dhidi ya wale watano. 10 Sasa Bonde la Sidimu lilikuwa limejaa mashimo ya lami, na wafalme wa Sodoma na Gomora walijaribu kutoroka lakini wakaanguka humo, na wale waliobaki wakakimbilia eneo lenye milima. 11 Kisha washindi wakachukua mali zote za Sodoma na Gomora na chakula chao chote na kwenda zao.+ 12 Pia wakamchukua Loti, mwana wa ndugu ya Abramu ambaye alikuwa akikaa Sodoma,+ na vilevile wakachukua mali zake, wakaenda zao.

13 Baada ya hayo mtu mmoja aliyetoroka akaja na kumletea habari Abramu Mwebrania. Wakati huo alikuwa akiishi karibu na miti mikubwa ya Mamre yule Mwamori,+ ndugu ya Eshkoli na Aneri.+ Wanaume hao walikuwa marafiki wa Abramu. 14 Hivyo Abramu akasikia kwamba mtu wake wa ukoo*+ alikuwa ametekwa. Kwa hiyo akawakusanya wanaume wake waliozoezwa, watumishi 318 waliozaliwa nyumbani mwake, wakawafuatia mpaka Dani.+ 15 Wakati wa usiku, akavigawa vikosi vyake, yeye na watumishi wake wakawashambulia na kuwashinda. Naye akawafuatia mpaka Hoba, upande wa kaskazini wa Damasko. 16 Alipata mali zote zilizochukuliwa, na pia akamwokoa Loti mtu wake wa ukoo, mali zake, wanawake, na watu wengine.

17 Abramu aliporudi baada ya kumshinda Kedorlaoma na wafalme waliokuwa pamoja naye, mfalme wa Sodoma alienda kukutana na Abramu kwenye Bonde la* Shave, yaani, Bonde la Mfalme.+ 18 Na Melkizedeki+ mfalme wa Salemu+ akaleta mkate na divai; alikuwa kuhani wa Mungu Aliye Juu Zaidi.+

19 Kisha akambariki Abramu na kumwambia:

“Abramu na abarikiwe na Mungu Aliye Juu Zaidi,

Muumba wa mbingu na dunia;

20 Na asifiwe Mungu Aliye Juu Zaidi,

Ambaye amewatia mikononi mwako wale wanaokukandamiza!”

Na Abramu akampa sehemu ya kumi ya vitu vyote.+

21 Baada ya hayo mfalme wa Sodoma akamwambia Abramu: “Nipe hao watu, lakini chukua mali.” 22 Lakini Abramu akamwambia mfalme wa Sodoma: “Ninauinua mkono wangu na kuapa kwa Yehova, Mungu Aliye Juu Zaidi, Muumba wa mbingu na dunia, 23 kwamba sitachukua kitu chochote ambacho ni chako, kuanzia uzi mpaka kamba ya kiatu, ili usije ukasema, ‘Nilimtajirisha Abramu.’ 24 Sitachukua chochote isipokuwa kile ambacho wanaume hawa vijana wamekula tayari. Lakini kuhusu fungu la watu walioenda pamoja nami, Aneri, Eshkoli, na Mamre+—acha wachukue fungu lao.”

15 Baada ya hayo neno la Yehova likamjia Abramu katika maono, likisema: “Usiogope,+ Abramu. Mimi ni ngao yako.+ Thawabu yako itakuwa kubwa sana.”+ 2 Abramu akasema: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, utanipa nini, kwa sababu mpaka sasa sina mtoto na yule atakayerithi nyumba yangu ni Eliezeri,+ mtu wa Damasko?” 3 Abramu akaendelea kusema: “Hujanipa uzao wowote,*+ na mtu* wa nyumba yangu atakuwa mrithi wangu.” 4 Lakini tazama! Yehova akamjibu hivi: “Mtu huyu hatakuwa mrithi wako, lakini mwana wako mwenyewe* atakuwa mrithi wako.”+

5 Ndipo akamtoa nje na kumwambia: “Tafadhali, tazama juu mbinguni uzihesabu nyota, ikiwa unaweza kuzihesabu.” Kisha akamwambia: “Ndivyo utakavyokuwa uzao wako.”*+ 6 Naye akawa na imani katika Yehova,+ Naye akamhesabu kuwa mwadilifu.*+ 7 Pia akasema hivi: “Mimi ni Yehova, niliyekutoa katika jiji la Uru la Wakaldayo ili nikupe nchi hii iwe miliki yako.”+ 8 Ndipo Abramu akauliza: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, nitajuaje kwamba nitaimiliki?” 9 Mungu akamjibu: “Chukua kwa ajili yangu ndama jike wa miaka mitatu, mbuzi jike wa miaka mitatu, kondoo dume wa miaka mitatu, njiwa tetere, na njiwa mchanga.” 10 Basi akawachukua wote hao na kuwakata vipande viwili na kuweka kila kipande kando ya kipande cha pili,* lakini hakuwakata ndege. 11 Kisha ndege wawindaji wakaanza kushuka juu ya mizoga hiyo, lakini Abramu akawa akiwafukuza.

12 Jua lilipokaribia kutua, usingizi mzito ukamshika Abramu na giza zito lenye kuogopesha likamfunika. 13 Kisha Mungu akamwambia Abramu: “Ujue kwa hakika kwamba wazao* wako watakuwa wageni katika nchi ambayo si yao na kwamba watu wa nchi hiyo watawafanya kuwa watumwa na kuwatesa kwa miaka 400.+ 14 Lakini mimi nitalihukumu taifa watakalolitumikia,+ na baada ya hapo watatoka huko na mali nyingi.+ 15 Lakini wewe, utaenda kwa mababu zako kwa amani; utazikwa baada ya kuishi maisha marefu.+ 16 Lakini wazao wako watarudi hapa+ katika kizazi cha nne, kwa sababu uovu wa Waamori bado haujafikia kipimo chake kamili.”+

17 Jua lilipotua na giza zito kuingia, tanuru linalofuka moshi lilitokea, na mwenge wa moto ukapita katikati ya vile vipande vya nyama. 18 Siku hiyo Yehova alifanya agano+ pamoja na Abramu, akisema: “Nitaupa uzao wako* nchi hii,+ kuanzia mto wa Misri mpaka kwenye ule mto mkubwa, mto Efrati:+ 19 nchi ya Wakeni,+ Wakenizi, Wakadmoni, 20 Wahiti,+ Waperizi,+ Warefaimu,+ 21 Waamori, Wakanaani, Wagirgashi, na Wayebusi.”+

16 Sasa Sarai mke wa Abramu hakuwa amemzalia mtoto yeyote,+ lakini alikuwa na mtumishi Mmisri aliyeitwa Hagari.+ 2 Basi Sarai akamwambia Abramu: “Sasa tafadhali! Yehova amenizuia nisizae watoto. Tafadhali, lala na mtumishi wangu. Huenda nikapata watoto kupitia yeye.”+ Kwa hiyo Abramu akasikiliza maneno ya Sarai. 3 Baada ya Abramu kuishi katika nchi ya Kanaani kwa miaka kumi, Sarai mke wa Abramu akamchukua Hagari, mtumishi wake Mmisri na kumpa Abramu mumewe awe mke wake. 4 Basi Abramu akalala na Hagari, naye akapata mimba. Alipogundua kwamba ana mimba, alianza kumdharau bimkubwa wake.

5 Ndipo Sarai akamwambia Abramu: “Ni wewe uliyesababisha madhara ninayotendewa. Ni mimi niliyemweka mtumishi wangu mikononi mwako,* lakini alipogundua kwamba ana mimba, alianza kunidharau. Yehova na awe mwamuzi kati yangu na wewe.” 6 Basi Abramu akamwambia Sarai: “Tazama! Mtumishi wako yuko chini ya mamlaka yako. Mtendee lolote unaloona ni jema.” Kisha Sarai akamfedhehesha Hagari, naye akamkimbia.

7 Baadaye malaika wa Yehova akamkuta kwenye chemchemi ya maji nyikani, chemchemi iliyo njiani kuelekea Shuri.+ 8 Naye akamuuliza: “Hagari, mtumishi wa Sarai, umetoka wapi na unaenda wapi?” Ndipo akajibu: “Ninamkimbia Sarai, bimkubwa wangu.” 9 Basi malaika wa Yehova akamwambia: “Rudi kwa bimkubwa wako na ujinyenyekeze chini ya mkono wake.” 10 Kisha malaika wa Yehova akasema: “Nitawazidisha sana wazao wako, hivi kwamba watakuwa wengi sana wasiweze kuhesabiwa.”+ 11 Malaika wa Yehova akaendelea kusema: “Sasa una mimba, nawe utazaa mwana, nawe unapaswa kumpa jina Ishmaeli,* kwa maana Yehova amesikia mateso yako. 12 Atakuwa mtu aliye kama pundamwitu.* Mkono wake utapigana na kila mtu, na mkono wa kila mtu utapigana naye, naye atakaa akielekeana na ndugu zake wote.”*

13 Ndipo akaliitia jina la Yehova, aliyekuwa akizungumza naye: “Wewe ni Mungu anayeona,”+ kwa kuwa alisema: “Je, ni kweli kwamba nimemwona hapa yeye ambaye huniona?” 14 Ndiyo sababu kisima hicho kiliitwa Beer-lahai-roi.* (Kiko kati ya Kadeshi na Beredi.) 15 Basi Hagari akamzalia Abramu mwana, naye Abramu akamwita huyo mwanawe ambaye Hagari alimzaa, Ishmaeli.+ 16 Abramu alikuwa na umri wa miaka 86 Hagari alipomzaa Ishmaeli.

17 Abramu alipokuwa na umri wa miaka 99, Yehova alimtokea na kumwambia: “Mimi ni Mungu Mweza-Yote. Tembea mbele zangu na ujithibitishe mwenyewe kuwa bila kosa.* 2 Nitaimarisha agano langu kati yangu na wewe,+ nami nitawafanya wazao wako wawe wengi, wengi sana.”+

3 Ndipo Abramu akaanguka kifudifudi, na Mungu akaendelea kuongea naye, na kumwambia: 4 “Mimi nami, tazama! agano langu liko pamoja nawe,+ nawe hakika utakuwa baba wa mataifa mengi.+ 5 Jina lako halitakuwa tena Abramu;* jina lako litakuwa Abrahamu,* kwa sababu nitakufanya kuwa baba wa mataifa mengi. 6 Nitakufanya uwe na wazao wengi, wengi sana, nami nitakufanya uwe mataifa, na wafalme watatoka kwako.+

7 “Nami nitalishika agano langu nililofanya pamoja nawe+ na uzao wako* baada yako katika vizazi vyao vyote; hili ni agano la milele, ili niwe Mungu wako na Mungu wa uzao wako* baada yako. 8 Nami nitakupa wewe na uzao wako* baada yako nchi ambamo uliishi ukiwa mgeni+—nchi yote ya Kanaani—iwe miliki ya kudumu, nami nitakuwa Mungu wao.”+

9 Mungu akaendelea kumwambia Abrahamu: “Wewe nawe, unapaswa kushika agano langu, wewe na uzao wako* baada yako katika vizazi vyao vyote. 10 Hili ndilo agano langu nililofanya pamoja nawe, ambalo wewe na uzao wako* baada yako mtalishika: Kila mwanamume miongoni mwenu ni lazima atahiriwe.+ 11 Ni lazima mtahiri nyama ya magovi yenu, na jambo hilo litakuwa ishara ya agano kati yangu nanyi.+ 12 Katika vizazi vyenu vyote, kila mwanamume miongoni mwenu mwenye umri wa siku nane ni lazima atahiriwe,+ yeyote anayezaliwa nyumbani mwenu na yeyote ambaye si mmoja wa uzao wenu* na yeyote aliyenunuliwa kwa pesa kutoka kwa mgeni. 13 Kila mwanamume aliyezaliwa nyumbani mwenu na kila mwanamume aliyenunuliwa kwa pesa zenu ni lazima atahiriwe,+ na agano langu katika miili yenu litakuwa agano la kudumu. 14 Ikiwa mwanamume yeyote ambaye hajatahiriwa hatatahiri nyama ya govi lake, ni lazima auawe. Amevunja agano langu.”

15 Kisha Mungu akamwambia Abrahamu: “Kuhusu mke wako Sarai,*+ usimwite tena Sarai, kwa sababu jina lake litakuwa Sara.* 16 Nitambariki na pia nitakupa mwana kupitia yeye;+ nitambariki Sara, naye atakuwa mataifa; wafalme wa mataifa watatoka kwake.” 17 Ndipo Abrahamu akaanguka kifudifudi, akaanza kucheka na kusema moyoni mwake:+ “Je, mwanamume mwenye umri wa miaka 100 atazaa mtoto, na je, Sara, mwanamke mwenye umri wa miaka 90, atazaa?”+

18 Kwa hiyo Abrahamu akamwambia Mungu wa kweli: “Afadhali umbariki Ishmaeli ili aendelee kuishi!”+ 19 Ndipo Mungu akasema: “Mke wako Sara hakika atakuzalia mwana, nawe unapaswa kumpa jina Isaka.*+ Nami nitaimarisha agano langu pamoja naye liwe agano la milele kwa uzao wake* baada yake.+ 20 Lakini kuhusu Ishmaeli, nimesikia ombi lako. Tazama! Nitambariki, nami nitamfanya awe na wazao wengi, nao wataongezeka na kuwa wengi, wengi sana. Atazaa wakuu 12, nami nitamfanya awe taifa kubwa.+ 21 Hata hivyo, nitaimarisha agano langu pamoja na Isaka,+ ambaye Sara atakuzalia wakati huuhuu mwaka ujao.”+

22 Mungu alipomaliza kuzungumza na Abrahamu, alipanda na kumwacha Abrahamu. 23 Kisha Abrahamu akamchukua Ishmaeli mwana wake na wanaume wote waliozaliwa nyumbani mwake na kila mwanamume aliyekuwa amemnunua kwa pesa, kila mwanamume katika nyumba ya Abrahamu, naye akawatahiri nyama ya magovi yao siku hiyohiyo, kama Mungu alivyokuwa amemwambia.+ 24 Abrahamu alikuwa na umri wa miaka 99 alipotahiriwa nyama ya govi lake.+ 25 Na Ishmaeli mwanawe alikuwa na umri wa miaka 13 alipotahiriwa nyama ya govi lake.+ 26 Siku hiyohiyo, Abrahamu alitahiriwa na pia Ishmaeli mwanawe. 27 Wanaume wote wa nyumba yake, yeyote aliyezaliwa nyumbani mwake na yeyote aliyenunuliwa kwa pesa kutoka kwa mgeni, walitahiriwa pia pamoja naye.

18 Baadaye, Yehova*+ akamtokea kati ya miti mikubwa ya Mamre+ alipokuwa ameketi kwenye mlango wa hema mchana wakati wa joto kali. 2 Akainua macho yake na kuwaona wanaume watatu wakiwa wamesimama umbali fulani kutoka kwake.+ Alipowaona, alikimbia kutoka kwenye mlango wa hema na kwenda kuwapokea, naye akainama mpaka chini. 3 Kisha akasema: “Yehova, ikiwa nimepata kibali machoni pako, tafadhali usinipite mimi mtumishi wako. 4 Tafadhali, acheni maji kidogo yaletwe ili mwoshwe miguu yenu;+ kisha mpumzike chini ya mti. 5 Kwa sababu mmekuja hapa kwangu mimi mtumishi wenu, acheni nilete kipande cha mkate ili mjiburudishe.* Kisha mnaweza kuendelea na safari yenu.” Ndipo wakasema: “Ni sawa. Unaweza kufanya kama ulivyosema.”

6 Kwa hiyo Abrahamu akaenda haraka hemani na kumwambia Sara: “Fanya haraka! Chukua vipimo vitatu* vya unga laini, ukande unga huo, na kuoka mikate.” 7 Kisha Abrahamu akakimbia kwenda kwenye mifugo, akachagua ng’ombe dume mchanga, mzuri na laini. Akampa mtumishi wake, naye akafanya haraka kumtayarisha. 8 Halafu akachukua siagi na maziwa na huyo ng’ombe dume mchanga ambaye alikuwa amemtayarisha, akaviweka vyakula hivyo mbele yao. Kisha akasimama kando yao chini ya mti walipokuwa wakila.+

9 Wakamuuliza: “Yuko wapi Sara mke wako?”+ Akajibu: “Yumo humu hemani.” 10 Kwa hiyo mmoja wao akasema: “Kwa hakika nitarudi kwako mwaka ujao wakati huuhuu, na tazama! mke wako Sara atakuwa na mwana.”+ Sasa Sara alikuwa akisikiliza kwenye mlango wa hema uliokuwa nyuma ya mtu huyo. 11 Abrahamu na Sara walikuwa wazee, umri wao ulikuwa umesonga.+ Sara alikuwa amepita umri wa kuzaa watoto.*+ 12 Kwa hiyo Sara akaanza kucheka kimoyomoyo na kusema: “Nikiwa mkongwe hivi na bwana wangu akiwa amezeeka, ninaweza kweli kupata shangwe hii?”+ 13 Kisha Yehova akamwambia Abrahamu: “Kwa nini Sara amecheka na kusema, ‘Je, kweli nitazaa mtoto nikiwa nimezeeka?’ 14 Je, kuna jambo lolote lisilowezekana kwa Yehova?+ Nitarudi kwako mwaka ujao wakati huuhuu, na Sara atakuwa na mwana.” 15 Lakini Sara akakana akisema, “Mimi sikucheka!” kwa maana aliogopa. Ndipo Mungu akamwambia: “Hakika! Ulicheka.”

16 Wanaume hao waliposimama ili kuondoka Abrahamu aliwasindikiza, wakatazama chini kuelekea Sodoma.+ 17 Yehova akasema: “Kwa nini nimfiche Abrahamu jambo ninalokusudia kufanya?+ 18 Kwa hakika Abrahamu atakuwa taifa kubwa na lenye nguvu, na mataifa yote ya dunia yatabarikiwa* kupitia yeye.+ 19 Kwa maana sasa nimemjua ili awaamuru watoto wake na nyumba yake baada yake kushika njia ya Yehova kwa kutenda yaliyo sawa na ya haki,+ ili Yehova atimize mambo aliyoahidi kumhusu Abrahamu.”

20 Kisha Yehova akasema: “Kilio dhidi ya Sodoma na Gomora kwa kweli ni kikubwa,+ na dhambi yao ni nzito sana.+ 21 Nitashuka chini ili nione kama mambo wanayotenda yanalingana na kilio kilichonifikia. Na kama sivyo, nitajua.”+

22 Kisha wanaume hao wakatoka huko na kuelekea Sodoma, lakini Yehova+ akabaki na Abrahamu. 23 Kisha Abrahamu akamkaribia na kumuuliza: “Je, kweli utamfagilia mbali mwadilifu pamoja na mwovu?+ 24 Tuseme kuna watu 50 waadilifu katika jiji hilo. Je, kweli utawafagilia mbali na hutalisamehe jiji hilo kwa ajili ya waadilifu hao 50 waliomo? 25 Ni jambo usiloweza kuwazia kumuua mwadilifu pamoja na mwovu hivi kwamba mtu mwadilifu apatwe na jambo lilelile linalompata mwovu!+ Ni jambo usiloweza kuwazia.+ Je, Mwamuzi wa dunia yote hatatenda jambo la haki?”+ 26 Kisha Yehova akasema: “Nikipata watu 50 waadilifu katika jiji la Sodoma, nitalisamehe jiji lote kwa ajili yao.” 27 Lakini Abrahamu akasema tena: “Tafadhali, nimethubutu kuzungumza nawe, Yehova, ijapokuwa mimi ni mavumbi na majivu. 28 Tuseme waadilifu hao 50 wapungue watano. Je, utaliangamiza jiji lote kwa sababu ya hao watano?” Akajibu: “Sitaliangamiza nikipata waadilifu 45 humo.”+

29 Lakini kwa mara nyingine tena akamwambia: “Tuseme 40 wapatikane humo.” Akamjibu: “Sitaliangamiza kwa ajili ya hao 40.” 30 Lakini akaendelea kusema: “Tafadhali Yehova, usiwake hasira,+ niruhusu niendelee kuongea: Tuseme ni 30 tu wanaopatikana humo.” Akamjibu: “Sitaliangamiza nikipata 30 humo.” 31 Lakini akaendelea kusema: “Tafadhali, nimethubutu kuzungumza nawe, Yehova: Tuseme ni 20 tu wanaopatikana humo.” Mungu akamjibu: “Sitaliangamiza kwa ajili ya hao 20.” 32 Mwishowe akasema: “Tafadhali Yehova, usiwake hasira, lakini niruhusu niongee kwa mara ya mwisho: Tuseme ni kumi tu wanaopatikana humo.” Akamjibu: “Sitaliangamiza kwa ajili ya hao kumi.” 33 Yehova alipomaliza kuzungumza na Abrahamu, alienda zake+ na Abrahamu akarudi nyumbani kwake.

19 Wale malaika wawili wakafika Sodoma jioni, na Loti alikuwa ameketi katika lango la Sodoma. Loti alipowaona, akasimama ili awapokee, akainama chini kifudifudi.+ 2 Naye akasema: “Tafadhali, bwana zangu, tafadhali, karibuni nyumbani mwangu mimi mtumishi wenu, mlale hapa usiku wa leo, nasi tuioshe miguu yenu. Kisha mnaweza kuamka asubuhi na mapema na kuendelea na safari yenu.” Wakamwambia: “Hapana, tutakaa usiku kucha kwenye uwanja wa jiji.” 3 Lakini akawasihi sana hivi kwamba wakaingia pamoja naye ndani ya nyumba yake. Kisha akawaandalia karamu, akaoka mikate isiyo na chachu, nao wakala.

4 Kabla hawajalala, wanaume wa jiji—wanaume wa Sodoma kuanzia mvulana mpaka mzee, wote—wakaizingira nyumba hiyo wakiwa umati. 5 Nao walikuwa wakimwambia Loti kwa sauti: “Wako wapi wale wanaume waliokuja kwako usiku wa leo? Walete nje kwetu ili tufanye nao ngono.”+

6 Ndipo Loti akatoka nje kukutana nao mlangoni, naye akaufunga mlango nyuma yake. 7 Akasema: “Tafadhali, ndugu zangu, msitende uovu. 8 Tafadhali, humu nina mabinti wawili ambao hawajawahi kufanya ngono na mwanamume. Tafadhali, acheni niwalete nje kwenu muwatendee lolote mnaloona kuwa jema. Lakini msiwatendee lolote wanaume hawa, kwa sababu wamekuja chini ya kivuli cha* paa langu.”+ 9 Ndipo wakasema: “Ondoka!” Halafu wakasema: “Mgeni huyu aliye peke yake alikuja kuishi hapa, na sasa anathubutu kutuhukumu! Sasa tutakutendea wewe jambo baya zaidi kuliko wao.” Wakamzingira Loti na kumbana* na kusogea mbele ili wauvunje mlango. 10 Basi wale wanaume* wakanyoosha nje mikono yao na kumwingiza Loti ndani ya nyumba walimokuwa, nao wakafunga mlango. 11 Lakini wakawapiga kwa upofu wanaume waliokuwa mlangoni, kuanzia mdogo zaidi mpaka mkubwa zaidi, hivi kwamba wakajichosha wakijaribu kuutafuta mlango.

12 Kisha wale wanaume* wakamwambia Loti: “Je, una mtu mwingine yeyote hapa? Wakwe zako, wanao, mabinti wako, na watu wengine wote wa ukoo jijini, waondoe mahali hapa! 13 Kwa maana tutaliangamiza jiji hili, kwa sababu kilio dhidi ya wakaaji wake kwa kweli kimeongezeka sana* mbele za Yehova,+ hivi kwamba Yehova ametutuma tuliangamize jiji hili.” 14 Kwa hiyo Loti akatoka nje na kuanza kuzungumza na wakwe zake ambao wangewaoa mabinti zake, akawaambia tena na tena: “Ondokeni! Ondokeni mahali hapa, kwa sababu Yehova ataliangamiza jiji hili!” Lakini machoni pa wakwe zake alionekana kama mtu anayefanya mzaha.+

15 Kulipokuwa kukipambazuka, malaika wakaanza kumhimiza Loti kwa uharaka, wakisema: “Fanya haraka! Mchukue mke wako na mabinti wako wawili walio hapa pamoja nawe, ili usifagiliwe mbali pamoja na uovu wa jiji hili!”+ 16 Alipozidi kukawia, basi kwa sababu Yehova alimhurumia,+ wale wanaume* wakaushika mkono wake na mkono wa mke wake na mikono ya mabinti zake wawili, wakamtoa na kumpeleka nje ya jiji.+ 17 Mara tu walipokuwa wamewatoa nje ya jiji, mmoja wao akawaambia: “Kimbieni msije mkafa! Msitazame nyuma+ wala msisimame mahali popote katika wilaya hii!+ Kimbilieni eneo lenye milima msije mkafagiliwa mbali!”

18 Kisha Loti akawaambia: “Tafadhali Yehova,* acha nisiende huko! 19 Sasa tafadhali, mimi mtumishi wako nimepata kibali machoni pako, nawe unanionyesha fadhili nyingi* kwa kunihifadhi hai,+ lakini siwezi kukimbilia eneo lenye milima kwa sababu ninaogopa kwamba huenda msiba ukanikumba nami nikafa.+ 20 Sasa tafadhali, mji huu uko karibu nami ninaweza kukimbilia humo; ni mji mdogo tu. Tafadhali, ninaweza kukimbilia humo? Ni mji mdogo tu. Kisha nitaokoka.”* 21 Kwa hiyo akamwambia: “Sawasawa, nitakutendea pia kwa fadhili,+ sitauangamiza mji uliotaja.+ 22 Fanya haraka! Kimbilia huko, kwa sababu sitafanya jambo lolote mpaka utakapofika huko!”+ Ndiyo sababu aliuita mji huo Soari.*+

23 Jua lilikuwa limechomoza nchini Loti alipofika Soari. 24 Kisha Yehova akaleta mvua ya kiberiti na moto juu ya Sodoma na Gomora—ilitoka kwa Yehova, kutoka mbinguni.+ 25 Kwa hiyo akayaangamiza majiji hayo, naam, wilaya yote, pamoja na wakaaji wote wa majiji hayo na mimea yote.+ 26 Lakini mke wa Loti, aliyekuwa nyuma ya Loti, akaanza kutazama nyuma, naye akawa nguzo ya chumvi.+

27 Sasa Abrahamu akaamka asubuhi na mapema na kwenda mahali alipokuwa amesimama mbele za Yehova.+ 28 Alipotazama chini kuelekea Sodoma na Gomora na nchi yote ya wilaya hiyo, aliona jambo la kushangaza. Kulikuwa na moshi mzito uliokuwa ukipanda juu kutoka nchini kama moshi mzito wa tanuru!*+ 29 Kwa hiyo Mungu alipoyaangamiza majiji ya wilaya hiyo, Mungu alimkumbuka Abrahamu kwa kumtoa Loti katika majiji aliyoyaangamiza, ambamo Loti alikuwa akiishi.+

30 Baadaye Loti akapanda kutoka Soari pamoja na mabinti zake wawili na kuanza kuishi katika eneo lenye milima,+ kwa sababu aliogopa kuishi Soari.+ Kwa hiyo akaanza kuishi pangoni pamoja na mabinti zake wawili. 31 Na mzaliwa wa kwanza akamwambia mdogo: “Baba yetu amezeeka, na hakuna mwanamume yeyote nchini anayeweza kulala nasi kama ilivyo desturi ya dunia yote. 32 Basi, tumpe baba yetu divai anywe, kisha tulale naye na kuhifadhi uzao wa baba yetu.”

33 Basi usiku huo wakampa baba yao divai nyingi anywe; kisha mzaliwa wa kwanza akaingia ndani na kulala na baba yake, lakini baba yake hakujua wakati alipolala naye wala alipoondoka. 34 Kisha siku iliyofuata, mzaliwa huyo wa kwanza akamwambia mdogo: “Jana usiku nililala na baba yetu. Na tumpe divai anywe usiku wa leo pia. Kisha uingie ndani na kulala naye, ili tuhifadhi uzao wa baba yetu.” 35 Basi usiku huo pia wakampa baba yao divai nyingi anywe; kisha yule binti mdogo akaingia ndani na kulala naye, lakini baba yake hakujua wakati alipolala naye wala alipoondoka. 36 Kwa hiyo mabinti wote wawili wa Loti wakapata mimba kutoka kwa baba yao. 37 Mzaliwa wa kwanza alizaa mwana na kumpa jina Moabu.+ Yeye ndiye baba ya Wamoabu wa leo.+ 38 Yule mdogo pia alizaa mwana, akampa jina Ben-ami. Yeye ndiye baba ya Waamoni+ wa leo.

20 Sasa Abrahamu akaihamisha kambi yake kutoka huko+ na kwenda katika nchi ya Negebu, akaanza kuishi kati ya Kadeshi+ na Shuri.+ Alipokuwa akiishi* Gerari,+ 2 Abrahamu akasema tena kumhusu Sara mke wake: “Huyu ni dada yangu.”+ Kwa hiyo Abimeleki mfalme wa Gerari akaagiza Sara aletwe, naye akamchukua.+ 3 Baadaye, Mungu akamjia Abimeleki katika ndoto usiku na kumwambia: “Wewe ni kama mtu aliyekufa kwa sababu ya mwanamke huyu uliyemchukua,+ kwa maana ameolewa naye ni mke wa mwanamume mwingine.”+ 4 Hata hivyo, Abimeleki hakuwa amemkaribia.* Kwa hiyo akasema: “Yehova, je, utaliua taifa ambalo kwa kweli halina hatia?* 5 Je, yeye hakuniambia, ‘Huyu ni dada yangu,’ na mwanamke huyu pia hakuniambia, ‘Huyu ni ndugu yangu’? Nilifanya jambo hili kwa moyo mnyoofu na mikono isiyo na hatia.” 6 Kisha Mungu wa kweli akamwambia katika ndoto: “Ninajua kwamba ulifanya jambo hili kwa moyo mnyoofu, kwa hiyo nilikuzuia usinitendee dhambi. Ndiyo sababu sikukuruhusu umguse. 7 Sasa mrudishe mke wa mwanamume huyo, kwa maana mwanamume huyo ni nabii,+ atakuombea dua,+ nawe utaendelea kuishi. Lakini usipomrudisha, ujue kwamba kwa hakika utakufa, wewe na watu wako wote.”

8 Abimeleki akaamka asubuhi na mapema akawaita watumishi wake wote na kuwaambia mambo hayo yote, nao wakaogopa sana. 9 Kisha Abimeleki akamwita Abrahamu na kumwambia: “Ni jambo gani hili ulilotutendea? Nimekutendea dhambi gani hivi kwamba umeniletea mimi na ufalme wangu dhambi kubwa hivi? Jambo ulilonitendea si sawa.” 10 Na Abimeleki akaendelea kumwambia Abrahamu: “Ulikuwa na nia gani ulipofanya jambo hili?”+ 11 Abrahamu akasema: “Ni kwa sababu nilisema moyoni mwangu, ‘Hakika watu wa mahali hapa hawamwogopi Mungu, nao wataniua kwa sababu ya mke wangu.’+ 12 Na isitoshe, kwa kweli huyu ni dada yangu, binti ya baba yangu lakini si binti ya mama yangu, naye akawa mke wangu.+ 13 Kwa hiyo Mungu aliponifanya nitangetange kutoka katika nyumba ya baba yangu,+ nilimwambia mke wangu: ‘Hivi ndivyo utakavyonionyesha upendo mshikamanifu: Kila mahali tutakapokwenda, sema hivi kunihusu, “Huyu ni ndugu yangu.”’”+

14 Basi Abimeleki akachukua kondoo na ng’ombe na watumishi wa kiume na wa kike akampa Abrahamu, naye akamrudishia Abrahamu mke wake, Sara. 15 Pia Abimeleki akasema: “Tazama nchi yangu iko wazi mbele yako. Ishi popote unapopenda.” 16 Naye akamwambia Sara: “Tazama ninampa ndugu yako vipande 1,000 vya fedha.+ Ni ishara ya kwamba huna hatia* mbele ya wote walio pamoja nawe na mbele ya watu wote, nawe umeondolewa shutuma.” 17 Na Abrahamu akaanza kumwomba dua Mungu wa kweli, naye Mungu akamponya Abimeleki na mke wake na vijakazi wake, nao wakaanza kuzaa watoto; 18 kwa maana Yehova alikuwa amewafanya wanawake wote wa nyumba ya Abimeleki wawe tasa* kwa sababu ya Sara, mke wa Abrahamu.+

21 Yehova akamkumbuka Sara kama alivyokuwa amesema, na Yehova akamtendea Sara jambo alilokuwa amemwahidi.+ 2 Basi Sara akapata mimba+ Abrahamu akiwa mzee, akamzalia mwana wakati uleule ambao Mungu alikuwa amemwahidi Abrahamu.+ 3 Abrahamu akamwita Isaka, mwana huyo ambaye Sara alikuwa amemzalia.+ 4 Na Abrahamu akamtahiri Isaka mwanawe akiwa na umri wa siku nane, kama Mungu alivyokuwa amemwamuru.+ 5 Abrahamu alikuwa na umri wa miaka 100 Isaka mwanawe alipozaliwa. 6 Kisha Sara akasema: “Mungu ameniletea kicheko; kila mtu atakayesikia jambo hili atacheka pamoja nami.”* 7 Naye akaendelea kusema: “Ni nani angeweza kumwambia Abrahamu, ‘Kwa hakika Sara atanyonyesha watoto’? Hata hivyo, nimemzalia mwana katika uzee wake.”

8 Basi mtoto huyo akakua na kuachishwa kunyonya, Abrahamu akafanya karamu kubwa siku ambayo Isaka aliachishwa kunyonya. 9 Lakini Sara alikuwa akiona kwamba mwana ambaye Hagari+ Mmisri alimzalia Abrahamu, alikuwa akimdhihaki Isaka.+ 10 Kwa hiyo akamwambia Abrahamu: “Mfukuze kijakazi huyu na mwanawe, kwa maana mwana wa kijakazi huyu hatakuwa mrithi pamoja na mwanangu, pamoja na Isaka!”+ 11 Lakini jambo hilo alilomwambia Abrahamu kumhusu mwanawe, halikumpendeza kamwe Abrahamu.+ 12 Kisha Mungu akamwambia Abrahamu: “Usikasirishwe na jambo ambalo Sara anakuambia kuhusu mvulana huyo na kuhusu kijakazi wako. Msikilize,* kwa maana ule utakaoitwa uzao wako utapitia* kwa Isaka.+ 13 Na kuhusu mwana wa kijakazi wako,+ nitatokeza pia taifa kutoka kwake,+ kwa sababu yeye ni uzao wako.”*

14 Basi Abrahamu akaamka asubuhi na mapema, akachukua mkate na kiriba cha ngozi chenye maji na kumpa Hagari. Akamtwika vitu hivyo begani na kumwambia aende zake pamoja na mwanawe.+ Kwa hiyo Hagari akaondoka na kutangatanga katika nyika ya Beer-sheba.+ 15 Mwishowe maji yaliyokuwa ndani ya kiriba hicho cha ngozi yakaisha, naye akamsukuma mvulana huyo chini ya kichaka fulani. 16 Kisha akaenda na kuketi chini peke yake, karibu umbali ambao mshale hufika unaporushwa kwa upinde, kwa maana alisema: “Sitaki kumwona mvulana huyu akifa.” Kwa hiyo akaketi chini umbali fulani na kuanza kulia kwa sauti na kutokwa na machozi.

17 Ndipo Mungu akasikia sauti ya mvulana huyo,+ na malaika wa Mungu akamwita Hagari kutoka mbinguni na kumwambia:+ “Hagari, kwa nini unalia? Usiogope, kwa sababu Mungu amesikia sauti ya mwanao pale alipo. 18 Simama, mwinue mwanao na umshike kwa mkono wako, kwa maana nitamfanya kuwa taifa kubwa.”+ 19 Kisha Mungu akamfungua macho, naye akaona kisima cha maji, akaenda na kukijaza maji kile kiriba cha ngozi na kumnywesha mwanawe. 20 Na Mungu alikuwa pamoja na mvulana huyo+ alipoendelea kukua. Aliishi nyikani, akawa mpiga mishale. 21 Alienda kuishi katika nyika ya Parani,+ na mama yake akamtafutia mke kutoka katika nchi ya Misri.

22 Wakati huo Abimeleki akiwa pamoja na Fikoli mkuu wa jeshi lake akamwambia Abrahamu: “Mungu yuko pamoja nawe katika kila jambo unalofanya.+ 23 Basi sasa niapie hapa mbele za Mungu kwamba hutanitendea kwa udanganyifu mimi na watoto wangu na wazao wangu, na kwamba utanitendea kwa upendo mshikamanifu mimi na wakaaji wa nchi ambayo umekuwa ukiishi, kama nilivyokutendea kwa upendo mshikamanifu.”+ 24 Kwa hiyo Abrahamu akasema: “Ninaapa hivyo.”

25 Hata hivyo, Abrahamu akamlalamikia Abimeleki kuhusu kisima cha maji ambacho watumishi wa Abimeleki walikuwa wamechukua kwa nguvu.+ 26 Abimeleki akamwambia: “Sijui ni nani aliyefanya jambo hilo; hukuniambia jambo hilo, leo ndio ninasikia habari hizo.” 27 Ndipo Abrahamu akachukua kondoo na ng’ombe na kumpa Abimeleki, na wote wawili wakafanya agano. 28 Abrahamu alipowatenga wanakondoo jike saba kutoka katika kundi, 29 Abimeleki akamuuliza Abrahamu: “Kwa nini umewatenga hawa wanakondoo jike saba?” 30 Akamjibu: “Pokea hawa wanakondoo jike saba kutoka mkononi mwangu kama ushahidi kwamba mimi ndiye niliyechimba kisima hiki.” 31 Ndiyo maana alipaita mahali hapo Beer-sheba,*+ kwa sababu wote wawili walikuwa wamekula kiapo mahali hapo. 32 Kwa hiyo wakafanya agano+ huko Beer-sheba, kisha Abimeleki akaondoka pamoja na Fikoli mkuu wa jeshi lake, wakarudi katika nchi ya Wafilisti.+ 33 Baada ya hayo Abrahamu akapanda mti wa mwesheli huko Beer-sheba, na huko akaliitia jina la Yehova,+ Mungu wa milele.+ 34 Naye Abrahamu akaishi* katika nchi ya Wafilisti kwa muda mrefu.*+

22 Sasa baada ya mambo hayo Mungu wa kweli akamjaribu+ Abrahamu, akamwambia: “Abrahamu!” akajibu: “Mimi hapa!” 2 Kisha Mungu akamwambia: “Tafadhali, mchukue mwana wako, mwana wako wa pekee unayempenda sana,+ Isaka,+ usafiri kwenda katika nchi ya Moria+ nawe umtoe kuwa dhabihu ya kuteketezwa juu ya mlima mmoja nitakaokuonyesha.”

3 Kwa hiyo Abrahamu akaamka asubuhi na mapema, akaweka matandiko juu ya punda wake na kuchukua wawili kati ya watumishi wake pamoja na Isaka mwanawe. Akapasua kuni kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa, kisha akafunga safari kwenda mahali ambapo Mungu wa kweli alimwonyesha. 4 Siku ya tatu, Abrahamu aliinua macho, akapaona mahali hapo kwa mbali. 5 Sasa Abrahamu akawaambia watumishi wake: “Ninyi kaeni hapa pamoja na punda, lakini mimi na mvulana huyu tutaenda kule ili kuabudu, halafu tutarudi.”

6 Kwa hiyo Abrahamu akachukua kuni kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa na kumtwika Isaka mwanawe. Halafu akabeba moto na kisu* mikononi, na wote wawili wakaendelea kutembea pamoja. 7 Kisha Isaka akamwambia Abrahamu baba yake: “Baba!” Akajibu: “Naam, mwanangu!” Halafu Isaka akauliza: “Hapa kuna moto na kuni, lakini yuko wapi kondoo kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa?” 8 Abrahamu akajibu: “Mwanangu, Mungu mwenyewe ataandaa kondoo kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa.”+ Na wote wawili wakaendelea kutembea.

9 Mwishowe wakafika mahali ambapo Mungu wa kweli alikuwa amemwonyesha, Abrahamu akajenga madhabahu hapo na kupanga kuni juu yake. Akamfunga Isaka mwanawe mikono na miguu na kumlaza kwenye madhabahu juu ya zile kuni.+ 10 Kisha Abrahamu akaunyoosha mkono wake na kuchukua kisu* ili amuue mwanawe.+ 11 Lakini malaika wa Yehova akamwita kutoka mbinguni: “Abrahamu, Abrahamu!” naye akajibu: “Mimi hapa!” 12 Kisha akasema: “Usimdhuru mvulana huyo, wala usimtendee lolote, kwa maana sasa ninajua kwamba unamwogopa Mungu kwa sababu hukuninyima+ mwana wako, mwana wako wa pekee.” 13 Ndipo Abrahamu akainua macho yake, na hapo karibu mbele yake kulikuwa na kondoo dume aliyenaswa kwa pembe zake kichakani. Kwa hiyo Abrahamu akaenda na kumchukua kondoo dume huyo na kumtoa dhabihu ya kuteketezwa badala ya mwanawe. 14 Naye Abrahamu akapaita mahali hapo Yehova-yire.* Ndiyo sababu mpaka leo inasemwa: “Katika mlima wa Yehova itaandaliwa.”+

15 Na malaika wa Yehova akamwita Abrahamu mara ya pili kutoka mbinguni, 16 akamwambia: “‘Naapa kwa nafsi yangu,’ asema Yehova,+ ‘kwamba kwa kuwa umetenda jambo hili nawe hujaninyima mwana wako, mwana wako wa pekee,+ 17 hakika nitakubariki, nami hakika nitaufanya uzao* wako uwe mwingi kama nyota za mbinguni na kama chembe za mchanga kwenye ufuo wa bahari,+ na uzao* wako utamiliki lango la* maadui wake.+ 18 Na kupitia uzao wako*+ mataifa yote ya dunia yatajipatia baraka kwa sababu umeisikiliza sauti yangu.’”+

19 Baada ya hayo Abrahamu akarudi kwa watumishi wake, wakaondoka wote pamoja na kurudi Beer-sheba;+ na Abrahamu akaendelea kuishi Beer-sheba.

20 Baadaye Abrahamu akaambiwa: “Tazama, Milka amemzalia pia Nahori ndugu yako+ wana hawa: 21 Usi mzaliwa wake wa kwanza, Buzi ndugu yake, Kemueli baba ya Aramu, 22 Kesedi, Hazo, Pildashi, Yidlafu, na Bethueli.”+ 23 Bethueli akamzaa Rebeka.+ Milka alimzalia Nahori ndugu ya Abrahamu wana hao wanane. 24 Suria wake, aliyeitwa Reuma, alimzalia pia wana hawa: Teba, Gahamu, Tahashi, na Maaka.

23 Na Sara aliishi miaka 127; hiyo ndiyo iliyokuwa miaka ya maisha ya Sara.+ 2 Basi Sara akafa huko Kiriath-arba,+ yaani, Hebroni,+ katika nchi ya Kanaani,+ naye Abrahamu akaanza kumwombolezea Sara na kumlilia. 3 Kisha Abrahamu akainuka na kutoka mahali ambapo maiti ya mke wake ilikuwepo, akawaambia wana wa Hethi:+ 4 “Mimi ni mgeni na mhamiaji miongoni mwenu.+ Nipeni ardhi ya kuzikia miongoni mwenu ili niweze kuwazika watu wangu waliokufa.” 5 Ndipo wana wa Hethi wakamwambia Abrahamu: 6 “Tusikilize, bwana wetu. Wewe ni kiongozi aliyechaguliwa na Mungu* miongoni mwetu.+ Unaweza kuwazika watu wako waliokufa mahali bora zaidi katika maeneo yetu ya kuzikia. Hakuna yeyote kati yetu atakayekunyima mahali pa kuwazika watu wako waliokufa.”

7 Basi Abrahamu akasimama na kuinama mbele ya wenyeji wa nchi, wana wa Hethi,+ 8 akawaambia: “Ikiwa mmekubali nimzike mtu wangu aliyekufa, basi nisikilizeni na mumsihi Efroni mwana wa Zohari 9 aniuzie pango lake la Makpela; liko ukingoni mwa shamba lake. Na aniuzie mbele yenu kwa kiasi kamili cha fedha+ ili niwe na mahali pa kuwazikia watu wangu.”+

10 Sasa Efroni alikuwa ameketi kati ya wana wa Hethi. Kwa hiyo Efroni Mhiti akamjibu Abrahamu mbele ya wana wa Hethi, na mbele ya wote walioingia katika lango la jiji,+ akasema: 11 “Hapana, bwana wangu! Nisikilize. Ninakupa shamba hilo pamoja na pango lililomo. Ninakupa mbele ya wana wa watu wangu. Mzike mtu wako aliyekufa.” 12 Ndipo Abrahamu akainama chini mbele ya wenyeji wa nchi 13 na kumwambia hivi Efroni mbele ya watu: “Tafadhali, nisikilize! Nitakupa kiasi kamili cha fedha kwa ajili ya shamba hilo. Zichukue kutoka mikononi mwangu, ili nimzike humo mtu wangu aliyekufa.”

14 Kisha Efroni akamwambia Abrahamu: 15 “Bwana wangu, nisikilize. Thamani ya shamba hili ni shekeli 400 za fedha,* lakini hiyo ni nini kati yangu na wewe? Mzike mtu wako aliyekufa.” 16 Abrahamu akamsikiliza Efroni, na Abrahamu akampimia Efroni kiasi cha fedha alichokuwa amemtajia mbele ya wana wa Hethi, shekeli 400 za fedha* kulingana na uzito uliokubaliwa na wafanyabiashara.+ 17 Kwa hiyo shamba la Efroni lililokuwa Makpela, mbele ya Mamre—shamba na pango lililokuwemo na miti yote iliyokuwa ndani ya mipaka ya shamba hilo—likathibitishwa kuwa 18 mali ya Abrahamu aliyoinunua mbele ya wana wa Hethi, mbele ya wote walioingia katika lango la jiji lake. 19 Baada ya hayo Abrahamu akamzika Sara mke wake katika pango la shamba la Makpela mbele ya Mamre, yaani, Hebroni, katika nchi ya Kanaani. 20 Hivyo wana wa Hethi wakamkabidhi Abrahamu lile shamba pamoja na pango lililokuwemo ili awazike watu wake humo.+

24 Sasa Abrahamu alikuwa amezeeka, umri wake ulikuwa umesonga, na Yehova alikuwa amembariki Abrahamu katika kila jambo.+ 2 Abrahamu akamwambia mtumishi wake, aliyekuwa na umri mkubwa zaidi nyumbani mwake, ambaye alisimamia mali zake zote:+ “Tafadhali, weka mkono wako chini ya paja langu, 3 nami nitakuapisha kwa jina la Yehova, Mungu wa mbingu na Mungu wa dunia, kwamba hutamchukulia mwanangu mke kutoka kwa mabinti wa Wakanaani, ninaoishi miongoni mwao.+ 4 Badala yake unapaswa kwenda katika nchi yangu na kwa watu wangu wa ukoo,+ ukamchukulie mke mwanangu Isaka.”

5 Lakini mtumishi huyo akamuuliza: “Namna gani mwanamke huyo akikataa kuja pamoja nami katika nchi hii? Je, nimrudishe mwana wako katika nchi uliyotoka?”+ 6 Ndipo Abrahamu akamwambia: “Hakikisha kwamba humpeleki mwanangu huko.+ 7 Yehova Mungu wa mbinguni, aliyenitoa katika nyumba ya baba yangu na kutoka katika nchi ya watu wangu wa ukoo+ na ambaye alizungumza nami na kuniapia:+ ‘Nitaupa uzao wako*+ nchi hii,’+ atamtuma malaika wake mbele yako,+ nawe hakika utamchukulia mwanangu mke kutoka huko.+ 8 Lakini ikiwa mwanamke huyo atakataa kuja pamoja nawe, utakuwa huru kutokana na kiapo hiki. Lakini usimpeleke mwanangu huko.” 9 Ndipo mtumishi huyo akaweka mkono wake chini ya paja la Abrahamu bwana wake na kumwapia kuhusu jambo hilo.+

10 Basi mtumishi huyo akachukua ngamia kumi kati ya ngamia wa bwana wake na kuondoka, akiwa na vitu vizuri vya kila aina kutoka kwa bwana wake. Kisha akaenda zake Mesopotamia, katika jiji la Nahori. 11 Akawapumzisha ngamia* kwenye kisima cha maji kilichokuwa nje ya jiji. Ilikuwa inaelekea jioni, wakati ambapo wanawake huenda kisimani kuteka maji. 12 Kisha akasema: “Yehova Mungu wa bwana wangu Abrahamu, tafadhali, nifanikishe leo, na umtendee kwa upendo wako mshikamanifu bwana wangu Abrahamu. 13 Nimesimama hapa kwenye chemchemi ya maji, na mabinti wa watu wa jiji wanakuja kuteka maji. 14 Na itukie kwamba msichana nitakayemwambia, ‘Tafadhali, ushushe mtungi wako ili ninywe maji,’ naye aseme, ‘Kunywa, nami nitawanywesha ngamia wako pia,’ na awe ndiye uliyemchagulia mtumishi wako, Isaka; na kwa jambo hilo acha nijue kwamba umemtendea bwana wangu kwa upendo wako mshikamanifu.”

15 Hata kabla hajamaliza kuongea, Rebeka, binti ya Bethueli+ mwana wa Milka+ mke wa Nahori,+ ndugu ya Abrahamu, akaja akiwa amebeba mtungi wa maji begani. 16 Basi msichana huyo alikuwa mrembo sana, bikira; hakuna mwanamume yeyote aliyekuwa amefanya ngono naye. Akateremka chini kwenye chemchemi, akaujaza maji mtungi wake, kisha akapanda kurudi. 17 Mara moja yule mtumishi akakimbia ili akutane naye, akamwambia: “Tafadhali, nipe maji kidogo ninywe kutoka kwenye mtungi wako.” 18 Msichana huyo akasema: “Kunywa, bwana wangu.” Ndipo akaushusha haraka mtungi wake na kuushikilia ili anywe maji. 19 Alipomaliza kumpa maji ya kunywa, akasema: “Nitateka pia maji kwa ajili ya ngamia wako mpaka watosheke.” 20 Kwa hiyo akamimina haraka maji ya mtungi wake ndani ya chombo cha kuwanyweshea wanyama, naye akakimbia tena na tena kisimani kuteka maji, akaendelea kuteka maji kwa ajili ya ngamia wake wote. 21 Wakati huo wote mwanamume huyo alikuwa kimya akimtazama kwa mshangao, akijiuliza kama Yehova alikuwa amefanikisha safari yake au la.

22 Ngamia walipotosheka kunywa maji, mwanamume huyo akatoa na kumpa pete ya puani ya dhahabu yenye uzito wa nusu shekeli* na bangili mbili za dhahabu zenye uzito wa shekeli kumi,* 23 kisha akamuuliza: “Tafadhali niambie, wewe ni binti ya nani? Kuna nafasi katika nyumba ya baba yako ambamo tunaweza kulala usiku huu?” 24 Akamjibu: “Mimi ni binti ya Bethueli+ mwana wa Milka, ambaye alimzalia Nahori.”+ 25 Akaendelea kusema: “Tuna nyasi na chakula kingi cha mifugo na pia mahali mnapoweza kulala usiku.” 26 Ndipo mwanamume huyo akainama chini na kusujudu mbele za Yehova 27 na kusema: “Yehova na asifiwe, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, kwa maana hajaacha kumtendea bwana wangu kwa upendo wake mshikamanifu na kwa uaminifu wake. Yehova ameniongoza mpaka kwenye nyumba ya ndugu za bwana wangu.”

28 Kisha msichana huyo akakimbia kuwaambia watu wa nyumbani mwa mama yake kuhusu mambo hayo. 29 Sasa Rebeka alikuwa na ndugu aliyeitwa Labani.+ Basi Labani akakimbia kwenda kukutana na huyo mwanamume aliyekuwa nje kwenye chemchemi. 30 Labani alipoona ile pete na zile bangili mikononi mwa dada yake na kuyasikia maneno ya Rebeka dada yake, ambaye alikuwa akisema, “Hivi ndivyo mwanamume huyo alivyoniambia,” Labani alikwenda kukutana na mwanamume huyo, ambaye bado alikuwa amesimama karibu na ngamia wake kando ya chemchemi. 31 Mara moja akamwambia: “Njoo, wewe uliyebarikiwa na Yehova. Kwa nini bado umesimama hapa nje? Nimekutayarishia nyumba na mahali kwa ajili ya ngamia wako.” 32 Ndipo mwanamume huyo akaingia ndani ya nyumba, naye* akawafungua ngamia na kuwapa nyasi na chakula cha mifugo na kuleta maji ya kuosha miguu yake na miguu ya wanaume waliokuwa pamoja naye. 33 Hata hivyo, chakula kilipowekwa mbele yake, alisema: “Sitakula mpaka niwaambie kilichonileta.” Kwa hiyo Labani akamwambia: “Tuambie!”

34 Kisha akasema: “Mimi ni mtumishi wa Abrahamu.+ 35 Na Yehova amembariki sana bwana wangu, na amemtajirisha sana kwa kumpa kondoo na ng’ombe, fedha na dhahabu, watumishi wa kiume na wa kike, na ngamia na punda.+ 36 Isitoshe, Sara, mke wa bwana wangu, akiwa amezeeka,+ alimzalia bwana wangu mwana, na bwana wangu atampa kila kitu alicho nacho.+ 37 Kwa hiyo bwana wangu aliniapisha hivi: ‘Usimchukulie mwanangu mke kutoka kwa mabinti wa Wakanaani ambao ninaishi katika nchi yao.+ 38 Hapana, bali utaenda katika nyumba ya baba yangu na katika ukoo wangu,+ nawe utamchukulia mwanangu mke kutoka huko.’+ 39 Lakini nikamuuliza bwana wangu: ‘Namna gani mwanamke huyo akikataa kuja pamoja nami?’+ 40 Akaniambia: ‘Yehova, ambaye nimetembea mbele zake,+ atamtuma malaika wake+ pamoja nawe, naye hakika ataifanikisha safari yako, nawe utamchukulia mwanangu mke kutoka katika ukoo wangu na kutoka katika nyumba ya baba yangu.+ 41 Utakuwa huru kutokana na kiapo chako ikiwa utaenda katika ukoo wangu nao wakatae kukupa msichana huyo. Hilo litakuweka huru kutokana na kiapo chako.’+

42 “Nilipofika kwenye chemchemi leo, nilisema: ‘Yehova Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ikiwa utaifanikisha safari yangu, 43 nimesimama kwenye kisima. Itatukia kwamba msichana+ akija kuteka maji nitasema, “Tafadhali, niruhusu ninywe maji kidogo kutoka katika mtungi wako,” 44 naye ataniambia, “Kunywa maji, na pia nitateka maji kwa ajili ya ngamia wako.” Mwanamke huyo na awe ndiye ambaye Yehova amemchagulia mwana wa bwana wangu.’+

45 “Kabla sijamaliza kusema maneno hayo moyoni mwangu, Rebeka akatokea akiwa amebeba mtungi begani, akateremka mpaka kwenye chemchemi na kuanza kuteka maji. Ndipo nikamwambia: ‘Tafadhali, nipe maji ninywe.’+ 46 Kwa hiyo akaushusha haraka mtungi wake kutoka begani mwake, akasema: ‘Kunywa maji,+ nami nitawanywesha pia ngamia wako.’ Basi nikanywa maji, naye akawanywesha pia ngamia wangu. 47 Baada ya hayo nikamuuliza, ‘Wewe ni binti ya nani?’ akajibu, ‘Binti ya Bethueli mwana wa Nahori, ambaye Milka alimzalia.’ Kwa hiyo nikamvisha pete puani na bangili mikononi mwake.+ 48 Nami nikainama chini na kusujudu mbele za Yehova na kumsifu Yehova Mungu wa bwana wangu Abrahamu,+ aliyekuwa ameniongoza kwenye njia inayofaa ili nimchukue binti ya ndugu ya bwana wangu kwa ajili ya mwana wake. 49 Na sasa niambieni ikiwa mnataka kumtendea bwana wangu kwa upendo mshikamanifu na uaminifu; lakini ikiwa sivyo, niambieni, ili nijue jambo la kufanya.”*+

50 Ndipo Labani na Bethueli wakajibu: “Jambo hili limetoka kwa Yehova. Hatuwezi kukuambia ndio au la.* 51 Rebeka ndiye huyu hapa. Mchukue uende, na awe mke wa mwana wa bwana wako, kama Yehova alivyosema.” 52 Mtumishi wa Abrahamu aliposikia maneno yao, mara moja akainama chini kifudifudi mbele za Yehova. 53 Na mtumishi huyo akaanza kutoa vito vya fedha na dhahabu na mavazi na kumpa Rebeka, naye akampa ndugu yake na mama yake vitu vyenye thamani. 54 Kisha mtumishi huyo na wanaume waliokuwa pamoja naye wakala na kunywa, nao wakalala huko usiku huo.

Alipoamka asubuhi alisema: “Niruhusuni niende kwa bwana wangu.” 55 Lakini ndugu na mama ya Rebeka wakamwambia: “Acha msichana huyu akae nasi kwa angalau siku kumi. Kisha anaweza kwenda.” 56 Lakini akawaambia: “Msinicheleweshe, kwa maana Yehova ameifanikisha safari yangu. Niruhusuni niondoke, ili niende kwa bwana wangu.” 57 Kwa hiyo wakasema: “Acha tumwite msichana huyo tumuulize.” 58 Wakamwita Rebeka na kumuuliza: “Je, utakwenda na mtu huyu?” Akajibu: “Niko tayari kwenda.”

59 Basi wakamruhusu Rebeka+ dada yao na mlezi wake*+ waende pamoja na mtumishi wa Abrahamu na watu wake. 60 Nao wakambariki Rebeka na kumwambia: “Dada yetu, na uwe maelfu mara elfu kumi,* na uzao wako umiliki* lango la* wale wanaowachukia.”+ 61 Kisha Rebeka na vijakazi wake wakainuka, wakapanda ngamia, na kumfuata mtumishi huyo. Kwa hiyo mtumishi huyo akamchukua Rebeka na kuondoka.

62 Sasa Isaka alikuwa ametoka upande wa Beer-lahai-roi,+ kwa maana alikuwa akiishi katika nchi ya Negebu.+ 63 Na Isaka alikuwa nje akitembea shambani akitafakari+ jioni giza linapokaribia kuingia. Alipoinua macho yake, tazama, aliona ngamia wakija! 64 Rebeka alipoinua macho, alimwona Isaka, akashuka haraka kutoka kwenye ngamia. 65 Kisha akamuuliza mtumishi wa Abrahamu: “Mwanamume yule anayetembea shambani akija kutupokea ni nani?” Mtumishi huyo akajibu: “Ni bwana wangu.” Kwa hiyo Rebeka akachukua shela yake na kujifunika. 66 Na mtumishi huyo akamwambia Isaka mambo yote aliyokuwa amefanya. 67 Kisha Isaka akampeleka Rebeka ndani ya hema la Sara mama yake.+ Hivyo akamchukua Rebeka, akawa mke wake; Isaka akampenda,+ akafarijika baada ya kifo cha mama yake.+

25 Kisha Abrahamu akaoa mke mwingine, naye aliitwa Ketura. 2 Baada ya muda Ketura akamzalia Abrahamu watoto hawa: Zimrani, Yokshani, Medani, Midiani,+ Ishbaki, na Shua.+

3 Yokshani akamzaa Sheba na Dedani.

Wana wa Dedani walikuwa Ashurimu, Letushimu, na Leumimu.

4 Wana wa Midiani walikuwa Efa, Eferi, Hanoki, Abida, na Eldaa.

Hao wote walikuwa wana wa Ketura.

5 Baadaye Abrahamu alimpa Isaka+ kila kitu alichokuwa nacho, 6 lakini Abrahamu akawapa zawadi wana wa masuria wake. Alipokuwa bado hai, akawaagiza waende upande wa mashariki, mbali na Isaka mwanawe,+ katika nchi ya Mashariki. 7 Abrahamu aliishi miaka 175. 8 Kisha Abrahamu akakata pumzi na kufa baada ya kuishi maisha marefu, akiwa amezeeka na kuridhika, naye akazikwa pamoja na watu wake.* 9 Isaka na Ishmaeli wanawe wakamzika katika pango la Makpela kwenye shamba la Efroni mwana wa Zohari Mhiti, lililo mbele ya Mamre,+ 10 shamba ambalo Abrahamu alinunua kutoka kwa wana wa Hethi. Abrahamu alizikwa huko pamoja na Sara mke wake.+ 11 Baada ya kifo cha Abrahamu, Mungu aliendelea kumbariki Isaka mwanawe,+ na Isaka alikuwa akikaa karibu na Beer-lahai-roi.+

12 Hii ndiyo historia ya Ishmaeli+ mwana wa Abrahamu ambaye Hagari+ Mmisri, kijakazi wa Sara, alimzalia Abrahamu.

13 Haya ndiyo majina ya wana wa Ishmaeli, kulingana na asili za koo zao: Nebayothi+ mzaliwa wa kwanza wa Ishmaeli, kisha Kedari,+ Adbeeli, Mibsamu,+ 14 Mishma, Duma, Masa, 15 Hadadi, Tema, Yeturi, Nafishi, na Kedema. 16 Hao ndio wana wa Ishmaeli, na hayo ndiyo majina yao kulingana na makao yao na kulingana na kambi zao,* wakuu 12 kulingana na koo zao.+ 17 Na Ishmaeli aliishi miaka 137. Kisha akakata pumzi na kufa, naye akazikwa pamoja na watu wake.* 18 Nao wakaanza kuishi katika nchi ya Havila+ karibu na Shuri,+ karibu na Misri, mpaka Ashuru. Aliishi karibu na ndugu zake wote.*+

19 Na hii ndiyo historia ya Isaka mwana wa Abrahamu.+

Abrahamu alimzaa Isaka. 20 Isaka alikuwa na umri wa miaka 40 alipomwoa Rebeka, binti ya Bethueli,+ Mwaramu wa Padan-aramu, dada ya Labani yule Mwaramu. 21 Naye Isaka akaendelea kumsihi Yehova kumhusu mke wake kwa sababu alikuwa tasa; kwa hiyo Yehova akasikiliza ombi lake, na Rebeka mke wake akapata mimba. 22 Na wana waliokuwa tumboni mwake wakaanza kupambana,+ akasema: “Ikiwa hivi ndivyo mambo yalivyo, kwa nini niendelee kuishi?” Basi akamuuliza Yehova kuhusu jambo hilo. 23 Yehova akamwambia: “Mataifa mawili yamo tumboni mwako,+ na mataifa mawili yatatenganishwa kutoka ndani yako;+ na taifa moja litakuwa na nguvu kuliko lingine,+ na mkubwa atamtumikia mdogo.”+

24 Wakati wake wa kuzaa ulipofika, tazama! mapacha walikuwa tumboni mwake. 25 Kisha wa kwanza akatoka, mwili wake wote ulikuwa mwekundu kama vazi la manyoya,+ kwa hiyo wakampa jina Esau.*+ 26 Kisha ndugu yake akatoka na mkono wake ulikuwa umeshika kisigino cha Esau,+ kwa hiyo akampa jina Yakobo.*+ Isaka alikuwa na umri wa miaka 60 Rebeka alipowazaa.

27 Wavulana hao walipoendelea kukua, Esau akawa mwindaji stadi,+ mtu wa mbugani, lakini Yakobo akawa mtu asiye na lawama, anayekaa katika mahema.+ 28 Na Isaka alimpenda Esau kwa sababu alikuwa akimletea nyama za porini, lakini Rebeka alimpenda Yakobo.+ 29 Siku moja Yakobo alipokuwa akichemsha mchuzi, Esau alirudi kutoka mbugani akiwa amechoka. 30 Kwa hiyo Esau akamwambia Yakobo: “Fanya haraka, tafadhali, nipe kiasi kidogo cha mchuzi huo mwekundu,* kwa maana nimechoka sana!”* Ndiyo sababu alipewa jina Edomu.*+ 31 Ndipo Yakobo akamwambia: “Kwanza niuzie haki yako ya mzaliwa wa kwanza!”+ 32 Esau akasema: “Ninakaribia kufa! Haki ya kuzaliwa ina faida gani kwangu?” 33 Yakobo akamwambia: “Niapie kwanza!” Basi akamwapia na kumuuzia Yakobo haki yake ya mzaliwa wa kwanza.+ 34 Ndipo Yakobo akampa Esau mkate na mchuzi wa dengu, akala na kunywa, kisha akainuka na kwenda zake. Hivyo, Esau akaidharau haki yake ya kuzaliwa.

26 Sasa kulikuwa na njaa kali nchini, mbali na ile njaa kali ya kwanza iliyotokea siku za Abrahamu,+ kwa hiyo Isaka akaenda Gerari kwa Abimeleki mfalme wa Wafilisti. 2 Kisha Yehova akamtokea Isaka na kumwambia: “Usishuke kwenda Misri. Kaa katika nchi nitakayokuonyesha. 3 Kaa kama mgeni katika nchi hii,+ nami nitaendelea kuwa pamoja nawe na kukubariki kwa sababu nitakupa wewe na uzao wako* nchi zote hizi,+ nami nitatimiza kiapo hiki nilichomwapia Abrahamu baba yako:+ 4 ‘Nitaufanya uzao* wako uwe mwingi kama nyota za mbinguni;+ nami nitaupa uzao* wako nchi zote hizi;+ na kupitia uzao* wako mataifa yote ya dunia yatajipatia baraka,’+ 5 kwa sababu Abrahamu aliisikiliza sauti yangu na kuendelea kutii matakwa yangu, amri zangu, maagizo yangu, na sheria zangu.”+ 6 Kwa hiyo Isaka akaendelea kuishi Gerari.+

7 Wanaume wa huko walipomuuliza kuhusu mke wake, alikuwa akisema: “Huyu ni dada yangu.”+ Aliogopa kusema, “Ni mke wangu,” kwa kuwa alisema, “Huenda wanaume hawa wakaniua kwa sababu ya Rebeka,” kwa maana alikuwa mrembo sana.+ 8 Baada ya muda kupita, Abimeleki mfalme wa Wafilisti alikuwa akiangalia nje dirishani, akamwona Isaka akimwonyesha mahaba* Rebeka mke wake.+ 9 Mara moja Abimeleki akamwita Isaka na kumwambia: “Kumbe ni mke wako! Mbona ulisema, ‘Huyu ni dada yangu’?” Isaka akamwambia: “Nilisema hivyo kwa sababu niliogopa nitauawa kwa sababu yake.”+ 10 Lakini Abimeleki akamuuliza: “Ni jambo gani hili ulilotutendea?+ Ingekuwa rahisi kwa yeyote kulala na mke wako, nawe ungetuletea hatia!”+ 11 Ndipo Abimeleki akawaamuru watu wote akisema: “Yeyote atakayemgusa mtu huyu na mke wake hakika atauawa!”

12 Na Isaka akaanza kupanda mbegu katika nchi hiyo, na mwaka huo alivuna mara 100 zaidi ya mbegu alizopanda, kwa kuwa Yehova alikuwa akimbariki.+ 13 Mwanamume huyo akatajirika, naye akaendelea kupata ufanisi mpaka akawa tajiri sana. 14 Alipata makundi ya kondoo na makundi ya ng’ombe na kundi kubwa la watumishi,+ nao Wafilisti wakaanza kumwonea wivu.

15 Kwa hiyo Wafilisti wakachukua udongo na kuvifukia visima vyote ambavyo watumishi wa baba yake walikuwa wamechimba siku za Abrahamu.+ 16 Kisha Abimeleki akamwambia Isaka: “Ondoka katika eneo letu, kwa sababu umekuwa na nguvu nyingi kuliko sisi.” 17 Kwa hiyo Isaka akaondoka huko na kupiga kambi katika bonde* la Gerari+ na kuanza kuishi huko. 18 Na Isaka akavichimbua visima vilivyokuwa vimechimbwa katika siku za Abrahamu baba yake lakini ambavyo Wafilisti walivifukia baada ya Abrahamu kufa,+ akavipa majina yaleyale ambayo baba yake alivipa.+

19 Watumishi wa Isaka walipokuwa wakichimba bondeni,* walipata kisima cha maji safi. 20 Nao wachungaji wa Gerari wakaanza kugombana na wachungaji wa Isaka, wakisema: “Maji haya ni yetu!” Basi akakiita kisima hicho Eseki,* kwa sababu walikuwa wamegombana naye. 21 Nao wakaanza kuchimba kisima kingine, wakaanza kukigombania pia. Basi akakiita Sitna.* 22 Baadaye akaondoka huko na kuchimba kisima kingine, lakini hawakukigombania. Basi akakiita Rehobothi* na kusema: “Ni kwa sababu sasa Yehova ametupa nafasi ya kutosha naye ametufanya tuongezeke nchini.”+

23 Kisha akapanda kutoka huko na kwenda Beer-sheba.+ 24 Yehova akamtokea usiku huo na kumwambia: “Mimi ni Mungu wa Abrahamu baba yako.+ Usiogope,+ kwa maana niko pamoja nawe, nami nitakubariki na kufanya uzao* wako uwe mwingi kwa sababu ya Abrahamu mtumishi wangu.”+ 25 Basi akajenga madhabahu huko na kuliitia jina la Yehova.+ Na Isaka akapiga hema lake huko,+ na watumishi wake wakachimba kisima huko.

26 Baadaye Abimeleki akamtembelea kutoka Gerari akiwa pamoja na Ahuzathi mshauri wake na Fikoli mkuu wa jeshi lake.+ 27 Basi Isaka akawauliza: “Kwa nini mmenitembelea, ilhali mlinichukia na kunifukuza katika eneo lenu?” 28 Wakamwambia: “Tumeona wazi kwamba Yehova amekuwa pamoja nawe.+ Basi tukasema, ‘Tafadhali, na kuwe na kiapo cha wajibu kati yetu sisi na wewe, na tufanye agano pamoja nawe+ 29 kwamba hutatutendea jambo lolote baya kama vile ambavyo hatujakudhuru, kama ujuavyo tulikutendea mema tu na tulikuruhusu uende zako kwa amani. Sasa wewe ni mbarikiwa wa Yehova.’” 30 Kisha akawafanyia karamu, nao wakala na kunywa. 31 Asubuhi wakaamka mapema na kufanya kiapo kati yao.+ Kisha Isaka akawaruhusu waende zao, nao wakaondoka kwa amani.

32 Siku hiyo watumishi wa Isaka walikuja na kumwambia kuhusu kisima walichokuwa wamechimba,+ wakasema: “Tumepata maji!” 33 Kwa hiyo akakiita Shiba. Ndiyo sababu tangu siku hiyo jiji hilo linaitwa Beer-sheba.+

34 Esau alipokuwa na umri wa miaka 40, alimwoa Yudithi binti ya Beeri Mhiti na pia Basemathi binti ya Eloni Mhiti.+ 35 Walikuwa chanzo cha huzuni kubwa* kwa Isaka na Rebeka.+

27 Sasa Isaka alipozeeka na macho yake yalipokuwa yamedhoofika sana asiweze kuona, alimwita Esau+ mwanawe mkubwa na kumwambia: “Mwanangu!” Naye akamjibu: “Naam, baba!” 2 Isaka akamwambia: “Sasa nimezeeka. Sijui nitakufa lini. 3 Basi sasa hivi, tafadhali, chukua silaha zako, podo lako na upinde wako, uende mbugani ukaniwindie mnyama wa mwituni.+ 4 Kisha unipikie chakula kitamu ninachokipenda sana. Nami nitakila ili nikubariki kabla sijafa.”

5 Hata hivyo, Rebeka alikuwa akisikiliza Isaka alipokuwa akizungumza na Esau mwanawe. Kisha Esau akaenda mbugani kuwinda mnyama wa mwituni na kumleta.+ 6 Basi Rebeka akamwambia Yakobo mwanawe:+ “Nimetoka kumsikia baba yako akizungumza na ndugu yako Esau na kumwambia, 7 ‘Niletee nyama ya porini, unipikie chakula kitamu. Kisha unipe nile ili nikubariki mbele za Yehova kabla sijafa.’+ 8 Na sasa, mwanangu, sikiliza kwa makini na ufanye ninayokuagiza.+ 9 Tafadhali, nenda kundini uniletee wanambuzi wawili walio bora, ili nimpikie baba yako chakula kitamu, kama anavyopenda. 10 Kisha mpelekee baba yako ale, ili akubariki kabla hajafa.”

11 Yakobo akamwambia Rebeka mama yake: “Lakini Esau ndugu yangu ni mwanamume mwenye nywele nyingi,+ na ngozi yangu ni laini. 12 Itakuwaje baba akinigusa?+ Bila shaka ataona ninamdhihaki, nami nitajiletea laana badala ya baraka.” 13 Ndipo mama yake akamwambia: “Mwanangu, laana ambayo ingekupata na inipate mimi. Fanya tu ninayokwambia na uende, niletee wanambuzi hao.”+ 14 Basi akaenda, akawachukua na kumletea mama yake, na mama yake akapika chakula kitamu, kama tu baba yake alivyopenda. 15 Baada ya hayo Rebeka akaingia nyumbani na kuchukua mavazi bora zaidi ya Esau mwanawe mkubwa, akamvisha Yakobo mwanawe mdogo.+ 16 Pia akamvisha ngozi za wanambuzi hao mikononi na pia kwenye sehemu isiyo na nywele shingoni.+ 17 Kisha akampa Yakobo mwanawe chakula kitamu alichopika na mkate aliokuwa ameoka.+

18 Kwa hiyo akaingia kwa baba yake na kusema: “Baba!” naye akajibu: “Naam! Wewe ni nani, mwanangu?” 19 Yakobo akamwambia baba yake: “Mimi ni Esau mzaliwa wako wa kwanza.+ Nimefanya kama ulivyoniambia. Keti tafadhali, ule nyama niliyokupikia ili unibariki.”+ 20 Ndipo Isaka akamuuliza mwanawe: “Mwanangu, umepataje mawindo haraka sana hivyo?” Akajibu: “Ni kwa sababu Yehova Mungu wako aliniletea.” 21 Kisha Isaka akamwambia Yakobo: “Tafadhali mwanangu, karibia ili nikuguse, nijue ikiwa wewe kwa kweli ni mwanangu Esau au la.”+ 22 Kwa hiyo Yakobo akamkaribia Isaka baba yake, naye akamgusa, kisha akasema: “Sauti ni sauti ya Yakobo, lakini mikono ni mikono ya Esau.”+ 23 Hakumtambua kwa sababu mikono yake ilikuwa na nywele nyingi kama mikono ya Esau ndugu yake. Kwa hiyo akambariki.+

24 Kisha akamuuliza: “Je, kweli wewe ni mwanangu Esau?” akajibu: “Ni mimi.” 25 Halafu akamwambia: “Mwanangu, niletee nyama ya porini nile, kisha nitakubariki.” Kwa hiyo akamletea, naye akala, pia akamletea divai, naye akanywa. 26 Kisha Isaka baba yake akamwambia: “Njoo karibu, tafadhali, unibusu, mwanangu.”+ 27 Kwa hiyo akakaribia na kumbusu, akasikia harufu ya mavazi yake.+ Kisha akambariki na kusema:

“Tazama, harufu ya mwanangu ni kama harufu ya shamba ambalo Yehova amebariki. 28 Mungu wa kweli na akupe umande wa mbingu+ na udongo wenye rutuba duniani,+ na wingi wa nafaka na divai mpya.+ 29 Mataifa na yakutumikie, mataifa na yainame chini mbele yako. Uwe bwana juu ya ndugu zako, na wana wa mama yako na wainame chini mbele yako.+ Alaaniwe kila mtu anayekulaani, na abarikiwe kila mtu anayekubariki.”+

30 Sasa Isaka alipomaliza tu kumbariki Yakobo na Yakobo alipotoka tu mbele ya Isaka baba yake, Esau ndugu yake akarudi kutoka mawindoni.+ 31 Yeye pia akapika chakula kitamu na kumletea baba yake, akamwambia baba yake: “Baba, amka ule nyama niliyokuletea, ili unibariki.” 32 Basi Isaka baba yake akamuuliza: “Wewe ni nani?” akamjibu: “Mimi ni mwana wako, mzaliwa wako wa kwanza, Esau.”+ 33 Kisha Isaka akaanza kutetemeka kwa nguvu sana, akasema: “Ni nani basi aliyewinda na kuniletea nyama? Tayari niliila kabla hujafika, nami nikambariki—naye hakika atabarikiwa!”

34 Aliposikia maneno ya baba yake, Esau akaanza kulia kwa sauti kubwa mno na kwa uchungu mwingi na kumwambia baba yake: “Nibariki mimi, naam, mimi pia, baba yangu!”+ 35 Lakini akamwambia: “Ndugu yako alikuja kwa udanganyifu ili apate baraka uliyopaswa kupata.” 36 Esau akamwambia: “Je, hiyo ndiyo sababu anaitwa Yakobo,* ili achukue nafasi yangu mara mbili?+ Tayari amechukua haki yangu ya mzaliwa wa kwanza,+ na sasa amechukua baraka yangu!”+ Kisha akauliza: “Hukuniachia baraka yoyote?” 37 Lakini Isaka akamjibu Esau: “Tazama, nimemweka awe bwana juu yako,+ nami nimempa ndugu zake wote wawe watumishi wake, nami nimempa nafaka na divai mpya ili kumtegemeza.+ Mwanangu, ni nini kilichobaki ninachoweza kukufanyia?”

38 Esau akamwambia baba yake: “Baba, je, una baraka moja tu? Nibariki mimi, naam, mimi pia, baba yangu!” Ndipo Esau akalia kwa sauti kubwa na kububujikwa na machozi.+ 39 Basi Isaka baba yake akamwambia:

“Tazama, makao yako yatakuwa mbali na udongo wenye rutuba duniani, na mbali na umande wa mbingu.+ 40 Na kwa upanga wako utaishi,+ nawe utamtumikia ndugu yako.+ Lakini utakaposhindwa kuvumilia, hakika utaivunja nira yake kutoka shingoni mwako.”+

41 Hata hivyo, Esau akawa na chuki kali dhidi ya Yakobo kwa sababu ya baraka ambayo baba yake alikuwa amempa,+ na Esau akawa akisema moyoni mwake: “Siku za kumwombolezea baba yangu zinakaribia.+ Zitakapokwisha nitamuua Yakobo ndugu yangu.” 42 Rebeka alipoambiwa maneno ya Esau mwana wake mkubwa, mara moja akaagiza Yakobo mwana wake mdogo aitwe, akamwambia: “Tazama! Esau ndugu yako anapanga kukuua ili kulipiza kisasi.* 43 Sasa mwanangu, fanya ninayokwambia. Ondoka, ukimbilie kwa Labani ndugu yangu kule Harani.+ 44 Ishi naye kwa muda mpaka ghadhabu ya ndugu yako itulie, 45 mpaka hasira ambayo ndugu yako anayo kukuelekea ipungue, naye asahau mambo uliyomtendea. Kisha nitatuma ujumbe ili urudi kutoka huko. Kwa nini niwapoteze nyote wawili siku moja?”

46 Baada ya hayo Rebeka akawa akimwambia Isaka: “Ninachukia maisha yangu kwa sababu ya mabinti wa Hethi.+ Yakobo akioa mke kutoka kwa mabinti wa Hethi, kama mabinti hawa wa nchi hii, maisha yangu yana faida gani?”+

28 Basi Isaka akamwita Yakobo, akambariki na kumwamuru hivi: “Usioe mke kutoka kwa mabinti wa Kanaani.+ 2 Nenda Padan-aramu katika nyumba ya Bethueli, baba ya mama yako, na uoe mke kutoka kwa mabinti wa Labani,+ ndugu ya mama yako. 3 Mungu Mweza-Yote atakubariki na kukufanya uwe na wazao wengi na kuongezeka, nawe hakika utakuwa kusanyiko la mataifa.+ 4 Naye atakupa wewe na uzao wako* baraka ambayo alimwahidi Abrahamu,+ ili uimiliki nchi ambamo umekuwa ukiishi kama mgeni, nchi ambayo Mungu alimpa Abrahamu.”+

5 Kwa hiyo Isaka akamruhusu Yakobo aondoke, naye akaenda Padan-aramu kwa Labani mwana wa Bethueli Mwaramu,+ ndugu ya Rebeka,+ mama ya Yakobo na Esau.

6 Esau akaona kwamba Isaka alikuwa amembariki Yakobo na kumwambia aende Padan-aramu kuoa mke kutoka huko na kwamba alipombariki, alimwamuru, “Usioe mke kutoka kwa mabinti wa Kanaani,”+ 7 na kwamba Yakobo alimtii baba yake na mama yake na kwenda Padan-aramu.+ 8 Ndipo Esau akatambua kwamba Isaka baba yake hakupendezwa na mabinti wa Kanaani,+ 9 kwa hiyo Esau akaenda kwa Ishmaeli mwana wa Abrahamu na kumwoa Mahalathi binti ya Ishmaeli, dada ya Nebayothi, kuongezea wake wengine aliokuwa nao.+

10 Yakobo akaondoka Beer-sheba na kuendelea na safari kuelekea Harani.+ 11 Baada ya muda akafika mahali fulani, akajitayarisha kulala hapo kwa sababu jua lilikuwa limetua. Kwa hiyo akachukua jiwe moja la mahali pale na kuliweka chini ili apumzishe kichwa chake juu yake, akalala hapo.+ 12 Kisha akaota ndoto, na tazama! Kulikuwa na ngazi iliyosimamishwa duniani, na kilele chake kilifika mpaka mbinguni; na kulikuwa na malaika wa Mungu waliokuwa wakipanda na kushuka kwenye ngazi hiyo.+ 13 Na tazama! Yehova alikuwa amesimama juu yake, naye akasema:

“Mimi ni Yehova Mungu wa Abrahamu baba yako na Mungu wa Isaka.+ Nchi unayoilalia, nitakupa wewe na uzao wako.*+ 14 Na hakika uzao wako utakuwa kama chembe za mavumbi ya ardhi,+ nawe utaenea mpaka upande wa magharibi na upande wa mashariki na upande wa kaskazini na upande wa kusini, na kupitia kwako na kupitia uzao wako familia zote duniani hakika zitabarikiwa.*+ 15 Niko pamoja nawe, nami nitakulinda popote utakapokwenda, nami nitakurudisha kwenye nchi hii.+ Sitakuacha mpaka nitakapofanya mambo niliyokuahidi.”+

16 Kisha Yakobo akaamka kutoka usingizini na kusema: “Kwa kweli Yehova yuko mahali hapa, nami sikujua.” 17 Naye akaogopa na kusema: “Mahali hapa panaogopesha kwelikweli! Bila shaka hapa ni nyumba ya Mungu,+ na hili ndilo lango la mbingu.”+ 18 Kwa hiyo Yakobo akaamka asubuhi na mapema na kuchukua lile jiwe alilokuwa amepumzisha kichwa chake juu yake, akalisimamisha kama nguzo na kumimina mafuta juu yake.+ 19 Basi akapaita mahali hapo Betheli,* lakini hapo awali jiji hilo liliitwa Luzi.+

20 Kisha Yakobo akaweka nadhiri hii: “Ikiwa Mungu ataendelea kuwa pamoja nami na kunilinda katika safari yangu na kunipa mkate wa kula na mavazi ya kuvaa 21 nami nirudi kwa amani katika nyumba ya baba yangu, kwa hakika Yehova atakuwa amethibitika kuwa Mungu wangu. 22 Na jiwe hili ambalo nimelisimamisha kama nguzo litakuwa nyumba ya Mungu,+ nami sitakosa kukupa sehemu ya kumi ya vitu vyote utakavyonipa.”

29 Baada ya hayo Yakobo akaendelea na safari yake, akafika katika nchi ya watu wa Mashariki. 2 Basi akaona kisima shambani na makundi matatu ya kondoo yakiwa yamelala kando yake, kwa sababu kwa kawaida wachungaji waliwanywesha kondoo wao maji ya kisima hicho. Kulikuwa na jiwe kubwa lililofunika kisima hicho. 3 Makundi yote ya kondoo yalipokusanywa hapo, wachungaji walilibingirisha jiwe lililofunika kisima hicho, nao wakawanywesha kondoo, kisha wakakifunika tena kisima kwa jiwe hilo.

4 Basi Yakobo akawauliza: “Ndugu zangu, mmetoka wapi?” wakamjibu: “Tumetoka Harani.”+ 5 Akawauliza: “Je, mnamjua Labani+ mjukuu wa Nahori?”+ wakamjibu: “Ndio, tunamjua.” 6 Ndipo akawauliza: “Je, hajambo?” wakamjibu: “Hajambo. Ndiye yule Raheli+ binti yake anakuja na kondoo!” 7 Kisha akasema: “Bado ni adhuhuri. Si wakati wa kukusanya kondoo. Wanywesheni kondoo, kisha wapelekeni malishoni.” 8 Wakamwambia: “Haturuhusiwi kufanya hivyo mpaka makundi yote ya kondoo yakusanywe kisha jiwe libingirishwe kutoka juu ya kisima. Ndipo tutakapowanywesha kondoo.”

9 Alipokuwa akizungumza nao, Raheli akaja na kondoo wa baba yake, kwa maana alikuwa mchungaji. 10 Yakobo alipomwona Raheli binti ya Labani, ndugu ya mama yake, na kondoo wa Labani, mara moja Yakobo akakaribia na kulibingirisha jiwe linalofunika kisima, akawanywesha kondoo wa Labani ndugu ya mama yake. 11 Kisha Yakobo akambusu Raheli, akalia kwa sauti kubwa na kububujikwa na machozi. 12 Na Yakobo akaanza kumwambia Raheli kwamba yeye ni mtu wa ukoo wa* baba yake na kwamba yeye ni mwana wa Rebeka. Basi Raheli akakimbia na kwenda kumwambia baba yake.

13 Mara tu Labani+ aliposikia kuhusu Yakobo mwana wa dada yake, akakimbia kwenda kumpokea. Akamkumbatia na kumbusu na kumleta nyumbani kwake. Naye akaanza kumwambia Labani mambo hayo yote. 14 Labani akamwambia: “Kwa kweli wewe ni mfupa wangu na nyama yangu.”* Basi akakaa naye kwa mwezi mzima.

15 Kisha Labani akamwambia Yakobo: “Je, unitumikie bure kwa sababu tu wewe ni mtu wangu wa ukoo?*+ Niambie, ungependa mshahara wako uwe nini?”+ 16 Sasa Labani alikuwa na mabinti wawili. Yule mkubwa aliitwa Lea, na mdogo aliitwa Raheli.+ 17 Lakini macho ya Lea hayakuwa yaking’aa, lakini Raheli alikuwa mwanamke mwenye kuvutia sana, tena mrembo. 18 Yakobo alikuwa amempenda Raheli, kwa hiyo akasema: “Niko tayari kukutumikia kwa miaka saba ili nimpate Raheli binti yako mdogo.”+ 19 Labani akasema: “Ni afadhali nikupe wewe binti huyo kuliko kumpa mwanamume mwingine. Endelea kukaa nami.” 20 Basi Yakobo akamtumikia Labani kwa miaka saba ili ampate Raheli,+ lakini machoni pake miaka hiyo ilikuwa kama siku chache tu kwa sababu ya upendo aliokuwa nao kwa Raheli.

21 Kisha Yakobo akamwambia Labani: “Nipe mke wangu nilale naye kwa sababu siku zangu zimekwisha.” 22 Ndipo Labani akawakusanya wakaaji wote wa eneo hilo na kufanya karamu. 23 Lakini wakati wa jioni, akamchukua Lea binti yake na kumleta kwa Yakobo ili alale naye. 24 Pia, Labani akamchukua Zilpa kijakazi wake na kumpa Lea binti yake ili awe kijakazi wake.+ 25 Asubuhi Yakobo akagundua kwamba alipewa Lea! Kwa hiyo akamuuliza Labani: “Ni jambo gani hili ulilonitendea? Je, sikukutumikia ili nimpate Raheli? Kwa nini umenitendea hila?”+ 26 Labani akamjibu: “Si desturi yetu hapa kumwoza binti mdogo kabla ya yule aliyezaliwa kwanza. 27 Sherehekea juma la mwanamke huyu. Kisha utapewa mwanamke huyu mwingine ukinitumikia kwa miaka mingine saba.”+ 28 Yakobo akafanya hivyo, akasherehekea juma la mwanamke huyo, kisha akampa Raheli binti yake awe mke wake. 29 Isitoshe, Labani alimchukua Bilha+ kijakazi wake na kumpa Raheli binti yake ili awe kijakazi wake.+

30 Kisha Yakobo akalala pia na Raheli, naye alimpenda Raheli kuliko Lea, akamtumikia Labani kwa miaka mingine saba.+ 31 Yehova alipoona kwamba Lea hapendwi,* alimwezesha kupata mimba,*+ lakini Raheli alikuwa tasa.+ 32 Kwa hiyo Lea akapata mimba na kuzaa mwana, akampa jina Rubeni,*+ kwa maana alisema: “Ni kwa sababu Yehova ameyaona mateso yangu,+ kwa maana sasa mume wangu ataanza kunipenda.” 33 Akapata mimba tena na kuzaa mwana, kisha akasema: “Ni kwa sababu Yehova amesikiliza, kwa maana sikupendwa, kwa hiyo amenipa huyu pia.” Basi akampa jina Simeoni.*+ 34 Akapata mimba tena na kuzaa mwana, kisha akasema: “Mara hii mume wangu ataungana nami, kwa sababu nimemzalia wana watatu.” Kwa hiyo mwana huyo akapewa jina Lawi.*+ 35 Akapata mimba tena na kuzaa mwana, akasema: “Wakati huu nitamsifu Yehova.” Kwa hiyo akampa jina Yuda.*+ Kisha akaacha kuzaa.

30 Raheli alipoona kwamba hajamzalia Yakobo watoto, alimwonea wivu dada yake, akaanza kumwambia Yakobo: “Nipe watoto, la sivyo nitakufa.” 2 Ndipo hasira ya Yakobo ikawaka dhidi ya Raheli, akamwambia: “Je, nimechukua nafasi ya Mungu, ambaye amekuzuia kuzaa watoto?”* 3 Raheli akamwambia: “Ndiye huyu kijakazi wangu Bilha.+ Lala naye ili anizalie watoto,* na ili kupitia yeye, mimi pia nipate watoto.” 4 Basi akampa Bilha kijakazi wake awe mke wake, Yakobo akalala naye.+ 5 Bilha akapata mimba na baada ya muda akamzalia Yakobo mwana. 6 Raheli akasema: “Mungu amekuwa mwamuzi wangu, naye ameisikiliza pia sauti yangu, akanipa mwana.” Ndiyo sababu alimpa jina Dani.*+ 7 Bilha, kijakazi wa Raheli, akapata mimba tena na kumzalia Yakobo mwana wa pili. 8 Kisha Raheli akasema: “Nimepigana mieleka mikali sana na dada yangu. Na pia nimeibuka mshindi!” Kwa hiyo akampa jina Naftali.*+

9 Lea alipoona kwamba ameacha kuzaa, alimchukua Zilpa kijakazi wake na kumpa Yakobo awe mke wake.+ 10 Na Zilpa kijakazi wa Lea akamzalia Yakobo mwana. 11 Kisha Lea akasema: “Kwa neema!” Basi akampa jina Gadi.*+ 12 Kisha Zilpa kijakazi wa Lea, akamzalia Yakobo mwana wa pili. 13 Lea akasema: “Kwa furaha yangu! Kwa maana hakika mabinti watanitangaza kuwa mwenye furaha.”+ Basi akampa jina Asheri.*+

14 Sasa Rubeni+ alikuwa akitembea siku za mavuno ya ngano, akapata dudai shambani. Kwa hiyo akamletea Lea mama yake. Basi Raheli akamwambia Lea: “Tafadhali, nipe baadhi ya dudai za mwana wako.” 15 Lea akamwambia: “Unafikiri ni jambo dogo kumchukua mume wangu?+ Unataka pia kuchukua dudai za mwanangu?” Raheli akasema: “Ni sawa. Yakobo atalala nawe usiku wa leo ukinipa dudai za mwana wako.”

16 Yakobo alipokuwa akirudi kutoka shambani jioni, Lea alienda kumpokea, akamwambia: “Utalala nami kwa sababu nimekukodi kikamili kwa dudai za mwanangu.” Basi akalala naye usiku huo. 17 Na Mungu akamsikiliza Lea na kumjibu, naye akapata mimba na baada ya muda akamzalia Yakobo mwana wa tano. 18 Kisha Lea akasema: “Mungu amenipa mshahara wangu* kwa sababu nimempa mume wangu kijakazi wangu.” Kwa hiyo akampa jina Isakari.*+ 19 Lea akapata mimba tena na baada ya muda akamzalia Yakobo+ mwana wa sita. 20 Lea akasema: “Mungu amenipa mimi zawadi, naam, amenipa mimi zawadi nzuri. Hatimaye, mume wangu atanivumilia,+ kwa maana nimemzalia wana sita.”+ Basi akampa jina Zabuloni.*+ 21 Baadaye akazaa binti na kumpa jina Dina.+

22 Mwishowe Mungu akamkumbuka Raheli, na Mungu akamsikia na kumjibu kwa kumwezesha kupata mimba.*+ 23 Akapata mimba na kuzaa mwana. Akasema: “Mungu ameiondoa aibu yangu!”+ 24 Basi akampa mwana huyo jina Yosefu,*+ akisema: “Yehova ananiongezea mwana mwingine.”

25 Baada ya Raheli kumzaa Yosefu, mara moja Yakobo akamwambia Labani: “Niruhusu niondoke ili niende nyumbani, katika nchi yangu.+ 26 Nipe wake zangu na watoto wangu, ambao nimekutumikia ili niwapate, niende zangu, kwa maana unajua vema jinsi nilivyokutumikia.”+ 27 Labani akamwambia: “Ikiwa nimepata kibali machoni pako,—ishara za ubashiri zimenisaidia* kuelewa kwamba Yehova ananibariki kwa sababu yako.” 28 Kisha akasema: “Niambie mshahara wako, nami nitakulipa.”+ 29 Basi Yakobo akamwambia: “Unajua jinsi nilivyokutumikia na jinsi nilivyoitunza mifugo yako;+ 30 kabla sijaja ulikuwa na wanyama wachache, lakini sasa wameongezeka na kuwa wengi, naye Yehova amekubariki tangu nilipokuja. Basi nitaishughulikia lini nyumba yangu mwenyewe?”+

31 Kisha akamuuliza: “Nikupe nini?” Yakobo akajibu: “Usinipe chochote! Lakini ukinifanyia jambo hili moja, nitaendelea kuichunga mifugo yako na kuilinda.+ 32 Nitapita kati ya mifugo yako yote leo. Watenge kondoo wote wenye madoadoa na wenye mabakamabaka na kila mwanakondoo dume wa rangi ya kahawia na mbuzi jike yeyote mwenye madoadoa na mabakamabaka. Kuanzia sasa na kuendelea, watakuwa mshahara wangu.+ 33 Na uadilifu* wangu utathibitisha kazi yangu siku utakapokuja kuangalia mshahara wangu; na ikiwa nitakuwa na mbuzi jike yeyote ambaye hatakuwa na madoadoa au mabakamabaka na mwanakondoo yeyote dume ambaye hatakuwa na rangi ya kahawia, basi atakuwa ameibwa.”

34 Labani akasema: “Vema! Na iwe kama ulivyosema.”+ 35 Basi siku hiyo akawatenga mbuzi dume wenye mistarimistari na mabakamabaka na mbuzi jike wote wenye madoadoa na mabakamabaka, na kila mwanakondoo dume mwenye madoadoa meupe na wa rangi ya kahawia; akawapa wanawe ili wawatunze. 36 Baada ya hayo Labani akasafiri kwa siku tatu kwenda kuchunga mifugo mbali na Yakobo, naye Yakobo akabaki akichunga mifugo ya Labani iliyosalia.

37 Ndipo Yakobo akachukua fito mbichi za mti wa mlubna, mlozi, na mwaramoni, akazibambua ili madoa meupe yaonekane. 38 Kisha akaziweka zile fito alizobambua mbele ya mifugo, kwenye mitaro, kwenye vyombo vya kunyweshea, mahali ambapo wanyama walikuja kunywa maji, ili wazione fito hizo na kupata joto la kupandana wanapokuja kunywa maji.

39 Basi wanyama hao walipata joto na kupandana mbele ya fito hizo, nao walizaa wanyama wenye mistarimistari, madoadoa, na mabakamabaka. 40 Kisha Yakobo akawatenga wanakondoo dume, halafu akageuza wanyama wa Labani ili wawaangalie wanyama wenye mistarimistari na pia wanyama wote wa rangi ya kahawia kati ya mifugo ya Labani. Kisha akatenga mifugo yake, naye hakuichanganya na mifugo ya Labani. 41 Na kila mara wanyama wenye nguvu walipopata joto la kupandana, Yakobo aliweka zile fito kwenye mitaro ili wanyama hao wazione na kupata joto la kupandana. 42 Lakini wanyama walipokuwa dhaifu, hakuziweka fito hizo kwenye mitaro. Kwa hiyo sikuzote wanyama dhaifu walikuwa wa Labani, lakini wenye nguvu walikuwa wa Yakobo.+

43 Kwa hiyo Yakobo akatajirika sana, akawa na makundi makubwa ya wanyama na watumishi wa kiume na wa kike na ngamia na punda.+

31 Baada ya muda Yakobo akawasikia wana wa Labani wakisema: “Yakobo amechukua kila kitu cha baba yetu, amepata utajiri huu wote kutokana na mali+ ya baba yetu.” 2 Kila mara Yakobo alipomtazama Labani, alitambua kwamba mtazamo wake kumwelekea ulikuwa umebadilika.+ 3 Hatimaye Yehova akamwambia Yakobo: “Rudi kwenye nchi ya baba zako na kwa watu wako wa ukoo,+ nami nitaendelea kuwa pamoja nawe.” 4 Kisha Yakobo akatuma ujumbe kwa Raheli na Lea na kuwaambia waje malishoni alikokuwa akichunga mifugo yake, 5 akawaambia:

“Nimeona kwamba mtazamo wa baba yenu kunielekea umebadilika,+ lakini Mungu wa baba yangu amekuwa pamoja nami.+ 6 Ninyi wenyewe mnajua kwa hakika kwamba nimemtumikia baba yenu kwa nguvu zangu zote.+ 7 Na baba yenu amejaribu kunidanganya na kubadili mshahara wangu mara kumi; lakini Mungu hajamruhusu anidhuru. 8 Kila mara aliposema, ‘Wanyama wenye madoadoa watakuwa mshahara wako,’ kundi lote lilizaa wanyama wenye madoadoa; na aliposema, ‘Wanyama wenye mistarimistari watakuwa mshahara wako,’ kundi lote lilizaa wanyama wenye mistarimistari.+ 9 Kwa hiyo Mungu akaendelea kuchukua mifugo ya baba yenu na kunipa. 10 Siku moja wanyama walipopata joto la kupandana, niliinua macho yangu na kuona katika ndoto kwamba mbuzi dume waliokuwa wakipanda majike walikuwa wenye mistarimistari, mabakamabaka, na madoadoa.+ 11 Kisha malaika wa Mungu wa kweli akaniita katika ndoto hiyo, ‘Yakobo!’ nikajibu, ‘Mimi hapa.’ 12 Akaniambia, ‘Tafadhali inua macho yako, uone kwamba mbuzi dume wote wanaowapanda majike wana mistarimistari, mabakamabaka, na madoadoa, kwa maana nimeona mambo yote ambayo Labani anakutendea.+ 13 Mimi ni Mungu wa kweli wa Betheli,+ mahali ambapo uliitia nguzo mafuta na kuniwekea nadhiri.+ Sasa inuka, ondoka katika nchi hii, urudi kwenye nchi uliyozaliwa.’”+

14 Ndipo Raheli na Lea wakamuuliza: “Je, kuna urithi wowote uliobaki kwa ajili yetu katika nyumba ya baba yetu? 15 Je, haoni kwamba sisi ni wageni kwa sababu ametuuza na amekuwa akitumia pesa alizopewa kwa ajili yetu?+ 16 Utajiri wote ambao Mungu amechukua kutoka kwa baba yetu ni wetu na wa watoto wetu.+ Basi sasa, fanya kila kitu ambacho Mungu amekuambia ufanye.”+

17 Kwa hiyo Yakobo akainuka na kuwapandisha watoto wake na wake zake juu ya ngamia,+ 18 naye akaanza kuchukua mifugo yake yote na mali zote alizokusanya+ huko Padan-aramu, akaanza safari ya kwenda kwa Isaka baba yake katika nchi ya Kanaani.+

19 Sasa Labani alikuwa ameenda kuwakata manyoya kondoo wake, Raheli akaiba sanamu za terafimu*+ za baba yake.+ 20 Isitoshe, Yakobo akamshinda akili Labani, Mwaramu, kwa maana hakuwa amemwambia kwamba ataondoka. 21 Akatoroka na kuvuka ule Mto,*+ yeye pamoja na vyote alivyokuwa navyo. Kisha akaelekea kwenye eneo lenye milima la Gileadi.+ 22 Siku ya tatu, Labani akaambiwa kwamba Yakobo ametoroka. 23 Basi Labani akawachukua ndugu zake* na kumfuatia Yakobo kwa muda wa siku saba na kumfikia katika eneo lenye milima la Gileadi. 24 Ndipo Mungu akamtokea Labani Mwaramu+ katika ndoto wakati wa usiku+ na kumwambia: “Uwe mwangalifu kuhusu mambo utakayomwambia Yakobo, yawe mema au mabaya.”+

25 Basi Labani akamkaribia Yakobo alipokuwa amepiga hema lake mlimani; Labani alikuwa amepiga kambi na ndugu zake kwenye eneo lenye milima la Gileadi. 26 Labani akamuuliza Yakobo: “Umefanya nini? Kwa nini umenichezea akili na kuwachukua mabinti wangu kama mateka waliochukuliwa kwa upanga? 27 Kwa nini ulitoroka kwa siri, ukanichezea akili badala ya kuniambia? Ikiwa ungeniambia, ningekuaga kwa shangwe na nyimbo, kwa tari na kinubi. 28 Lakini hukunipa nafasi ya kuwabusu wajukuu* wangu na mabinti wangu. Umetenda kipumbavu. 29 Nina uwezo wa kuwadhuru, lakini Mungu wa baba yenu aliongea nami usiku wa kuamkia leo, akaniambia, ‘Uwe mwangalifu kuhusu mambo utakayomwambia Yakobo, yawe mema au mabaya.’+ 30 Sasa umeondoka kwa sababu umekuwa ukitamani sana kurudi kwenye nyumba ya baba yako, lakini kwa nini umeiba miungu yangu?”+

31 Yakobo akamjibu Labani: “Ni kwa sababu niliogopa, kwa maana nilisema moyoni mwangu, ‘Huenda ukaninyang’anya kwa nguvu mabinti wako.’ 32 Yeyote utakayempata na miungu yako, atauawa. Pekua vitu nilivyo navyo mbele ya hawa ndugu zetu, uchukue chochote kilicho chako.” Lakini Yakobo hakujua kwamba Raheli alikuwa ameiba miungu hiyo. 33 Kwa hiyo Labani akaingia katika hema la Yakobo na hema la Lea na hema la wale vijakazi wawili,+ lakini hakuipata. Kisha akatoka katika hema la Lea na kuingia katika hema la Raheli. 34 Raheli alikuwa amechukua sanamu hizo za terafimu na kuziweka ndani ya kikapu cha wanawake kilicho kwenye matandiko ya ngamia na kuzikalia. Basi Labani alizitafuta kabisa katika hema lote lakini hakuzipata. 35 Ndipo Raheli akamwambia baba yake: “Bwanangu, usikasirike, kwa sababu siwezi kusimama mbele yako, kwa maana niko katika siku zangu za hedhi.”*+ Kwa hiyo akaendelea kuzitafuta kwa makini lakini hakuzipata sanamu hizo za terafimu.+

36 Ndipo Yakobo akakasirika na kuanza kumshutumu Labani. Akamuuliza Labani: “Nimefanya kosa gani, nimetenda dhambi gani hivi kwamba unanifuatia kwa bidii hivi? 37 Sasa kwa kuwa umepekua kabisa vitu vyangu vyote, umepata nini cha nyumba yako? Kiweke hapa mbele ya ndugu zangu na ndugu zako, waache waamue ni nani mwenye kosa kati yetu. 38 Kwa miaka hii 20 ambayo nimekaa nawe, mimba za kondoo wako na mbuzi wako hazikuharibika,+ wala sijawahi kula kondoo dume wa kundi lako. 39 Sijawahi kukuletea mnyama yeyote aliyeraruliwa na mnyama wa mwituni.+ Mimi mwenyewe nililipia hasara hiyo. Ulidai malipo kutoka kwangu kwa ajili ya mnyama yeyote aliyeibiwa mchana au usiku. 40 Jua lilinichoma wakati wa mchana na baridi ilinipiga usiku, na macho yangu yalipoteza usingizi.+ 41 Ilikuwa hivyo kwa miaka 20 niliyokaa nyumbani mwako. Nimekutumikia kwa miaka 14 ili niwapate mabinti wako wawili na kuchunga mifugo yako kwa miaka 6, nawe ulibadili tena na tena mshahara wangu mara kumi.+ 42 Ikiwa Mungu wa baba yangu,+ Mungu wa Abrahamu, Yule ambaye Isaka anamwogopa,*+ hangekuwa pamoja nami, sasa ungeniambia niende zangu mikono mitupu. Mungu ameyaona mateso yangu na kazi ngumu ya mikono yangu, na ndiyo sababu alikukaripia usiku wa kuamkia leo.”+

43 Labani akamwambia Yakobo: “Mabinti hawa ni mabinti wangu na watoto hawa ni watoto wangu na wanyama hawa ni wanyama wangu, na kila kitu unachoona hapa ni changu na cha mabinti wangu. Ni jambo gani ninaloweza kufanya leo kuwadhuru mabinti hawa au kuwadhuru watoto wao ambao wamewazaa? 44 Sasa njoo, tufanye agano kati yetu, wewe na mimi, nalo litakuwa ushahidi kati yetu.” 45 Basi Yakobo akachukua jiwe na kulisimamisha kama nguzo.+ 46 Kisha Yakobo akawaambia ndugu zake: “Okoteni mawe!” Basi wakaokota mawe na kutengeneza rundo la mawe. Halafu wakala chakula juu ya rundo hilo la mawe. 47 Na Labani akaanza kuliita rundo hilo Yegar-sahadutha,* lakini Yakobo akaliita Galeedi.*

48 Ndipo Labani akasema: “Rundo hili la mawe ni ushahidi kati yangu mimi na wewe leo.” Ndiyo sababu aliliita Galeedi,+ 49 na Mnara wa Mlinzi, kwa sababu alisema: “Yehova na awe mlinzi kati yangu mimi na wewe tunapokuwa hatuonani. 50 Ukiwatesa mabinti wangu na kuanza kuoa wake wengine kuongezea mabinti wangu, hata mwanadamu asipoona jambo hilo, kumbuka kwamba Mungu atakuwa shahidi kati yangu mimi na wewe.” 51 Labani akaendelea kumwambia Yakobo: “Hili hapa ni rundo la mawe, na hii hapa ni nguzo ambayo nimesimamisha kati yangu mimi na wewe. 52 Rundo hili la mawe ni ushahidi, na nguzo hii pia ni ushahidi+ kwamba sitapita rundo hili la mawe ili kuja kukudhuru, nawe hutapita rundo hili la mawe na nguzo hii ili kuja kunidhuru. 53 Mungu wa Abrahamu+ na Mungu wa Nahori, Mungu wa baba yao, na awe mwamuzi kati yetu.” Basi Yakobo akaapa kwa jina la Yule ambaye Isaka baba yake alimwogopa.*+

54 Kisha Yakobo akatoa dhabihu mlimani na kuwaalika ndugu zake wale chakula.* Wakala na kulala mlimani usiku huo. 55 Hata hivyo, Labani akaamka asubuhi na mapema, akawabusu wajukuu wake+ na mabinti zake na kuwabariki.+ Kisha Labani akaondoka, akarudi nyumbani.+

32 Kisha Yakobo akaendelea na safari yake, na malaika wa Mungu wakakutana naye. 2 Mara tu alipowaona, Yakobo akasema: “Hii ni kambi ya Mungu!” Kwa hiyo akapaita mahali hapo Mahanaimu.*

3 Kisha Yakobo akawatuma wajumbe wamtangulie kwenda kwa Esau ndugu yake katika nchi ya Seiri,+ katika eneo* la Edomu,+ 4 akawaamuru hivi: “Hivi ndivyo mtakavyomwambia bwana wangu, Esau, ‘Mtumishi wako Yakobo anasema hivi: “Nimeishi* na Labani kwa muda mrefu mpaka sasa.+ 5 Nami nimepata ng’ombe dume, punda, kondoo, na watumishi wa kiume na wa kike,+ nami ninakutumia ujumbe huu bwana wangu, ili nipate kibali machoni pako.”’”

6 Baada ya muda wajumbe hao wakarudi kwa Yakobo na kumwambia: “Tulikutana na ndugu yako Esau, naye yuko njiani, anakuja kukutana nawe akiwa na wanaume 400.”+ 7 Ndipo Yakobo akaogopa sana na kushikwa na wasiwasi.+ Basi akawagawa katika kambi mbili watu aliokuwa nao, na pia ng’ombe, ngamia, na mifugo mingine. 8 Akasema: “Esau akiishambulia kambi moja, kambi nyingine itaponyoka.”

9 Kisha Yakobo akasema: “Ee Mungu wa baba yangu Abrahamu na Mungu wa baba yangu Isaka, Ee Yehova, wewe unayeniambia, ‘Rudi kwenye nchi yako na kwa watu wako wa ukoo, nami nitakutendea mema,’+ 10 mimi sistahili upendo wote mshikamanifu na uaminifu wote ambao umenitendea mimi, mtumishi wako,+ kwa maana nilivuka mto huu wa Yordani nikiwa na fimbo yangu tu lakini sasa nina kambi mbili.+ 11 Nakuomba uniokoe+ kutoka mikononi mwa ndugu yangu Esau, kwa maana naogopa kwamba anaweza kuja kunishambulia mimi,+ na pia akina mama na watoto wao. 12 Lakini uliniambia: ‘Hakika nitakutendea mema, nami nitaufanya uzao* wako uwe mwingi kama chembe za mchanga wa bahari, zisizoweza kuhesabiwa kwa sababu ni nyingi sana.’”+

13 Naye Yakobo akalala huko usiku huo. Kisha akachukua baadhi ya mali zake ili ampe zawadi Esau ndugu yake:+ 14 mbuzi jike 200, mbuzi dume 20, kondoo jike 200, kondoo dume 20, 15 ngamia 30 wanaonyonyesha, ng’ombe 40, ng’ombe dume 10, punda jike 20, na punda dume 10 waliokomaa.+

16 Akawapa watumishi wake kundi moja baada ya lingine, akawaambia: “Nitangulieni mvuke kabla yangu, nanyi mwache nafasi kati ya kundi moja na kundi lingine.” 17 Pia akamwamuru hivi yule wa kwanza: “Ikiwa Esau ndugu yangu atakutana nawe na kukuuliza, ‘Wewe ni mtumishi wa nani, unaenda wapi, na wanyama hawa walio mbele yako ni wa nani?’ 18 utamwambia, ‘Ni mali ya mtumishi wako Yakobo. Ni zawadi aliyokutumia wewe, bwana wangu Esau,+ na tazama! yeye mwenyewe yuko nyuma anatufuata.’” 19 Akamwamuru hivi pia mtumishi wa pili, wa tatu, na wale wote waliokuwa wakiyafuata makundi hayo: “Mkikutana na Esau, mtamwambia maneno hayohayo. 20 Vilevile mtamwambia, ‘Mtumishi wako Yakobo yuko nyuma anatufuata.’” Kwa maana Yakobo alisema moyoni mwake: ‘Nikimtumia zawadi kwanza+ huenda nikamtuliza, na huenda atanipokea kwa fadhili nitakapokutana naye baadaye.’ 21 Kwa hiyo zawadi hizo zikavushwa na kupelekwa kwanza, lakini yeye mwenyewe akalala kambini usiku huo.

22 Baadaye usiku huo, akaamka na kuwachukua wake zake wawili+ na vijakazi wake wawili+ na wanawe wachanga 11 na kuvuka kivuko cha Yaboki.+ 23 Basi akawachukua na kuwavusha kwenye kijito,* akavusha pia vitu vingine vyote alivyokuwa navyo.

24 Mwishowe Yakobo akabaki peke yake. Kisha mwanamume fulani akaanza kupigana naye mweleka mpaka kulipopambazuka.+ 25 Mwanamume huyo alipoona kwamba hajamshinda Yakobo, akamgusa kiungio cha nyonga; na kiungio cha nyonga ya Yakobo kikateguka alipokuwa akipigana naye mweleka.+ 26 Kisha mwanamume huyo akasema: “Niache niende, kwa maana kunapambazuka.” Yakobo akamwambia: “Sitakuacha uende mpaka unibariki.”+ 27 Basi akamuuliza: “Jina lako ni nani?” akajibu: “Yakobo.” 28 Kisha akamwambia: “Jina lako halitakuwa tena Yakobo bali Israeli,*+ kwa maana umepambana na Mungu+ na wanadamu na hatimaye umeshinda.” 29 Naye Yakobo akamuuliza: “Tafadhali, niambie jina lako.” Hata hivyo, mwanamume huyo akamwambia: “Kwa nini unataka kujua jina langu?”+ Halafu akambariki huko. 30 Basi Yakobo akapaita mahali hapo Penieli,*+ kwa sababu alisema, “Nimemwona Mungu uso kwa uso, lakini uhai wangu umeokolewa.”*+

31 Na jua likachomoza mara tu Yakobo alipopita karibu na Penueli,* lakini alikuwa akichechemea kwa sababu ya nyonga yake.+ 32 Ndiyo maana tangu siku hiyo Waisraeli hawajazoea kula kano ya paja,* iliyo kwenye kiungio cha nyonga, kwa sababu mwanamume huyo aligusa kiungio cha nyonga ya Yakobo karibu na kano ya paja.

33 Sasa Yakobo akainua macho yake na kumwona Esau akija pamoja na wanaume 400.+ Kwa hiyo akawagawa watoto kati ya Lea, Raheli, na wale vijakazi wawili.+ 2 Akawaweka vijakazi na watoto wao mbele,+ kisha Lea na watoto wake,+ halafu Raheli+ na Yosefu nyuma yao. 3 Kisha yeye mwenyewe akaenda mbele yao, akainama mpaka chini mara saba huku akimkaribia ndugu yake.

4 Lakini Esau akakimbia kukutana naye, akamkumbatia na kumbusu, nao wakatokwa na machozi. 5 Alipoinua macho yake na kuona wanawake na watoto, akauliza: “Ni nani hawa walio pamoja nawe?” Yakobo akamwambia: “Ni watoto ambao Mungu amenipa kwa fadhili mimi mtumishi wako.”+ 6 Ndipo wale vijakazi wakaja mbele na watoto wao na kuinama chini, 7 Lea pia akaja mbele na watoto wake, nao wakainama chini. Kisha Yosefu akaja mbele na Raheli, nao wakainama chini.+

8 Esau akauliza: “Msafara huu wote ni wa nini?”+ Yakobo akamjibu: “Nimekuja ili kupata kibali machoni pako, bwana wangu.”+ 9 Esau akasema: “Nina mali nyingi sana, ndugu yangu.+ Usinipe mali zako.” 10 Lakini Yakobo akasema: “Hapana, tafadhali nakusihi. Ikiwa nimepata kibali machoni pako, pokea zawadi yangu kutoka mkononi mwangu, kwa sababu nimekuletea ili niuone uso wako. Nami nimeona uso wako kana kwamba nimeona uso wa Mungu, kwa maana umenipokea kwa furaha.+ 11 Tafadhali pokea zawadi yangu ya baraka uliyoletewa,+ kwa sababu Mungu amenibariki, nami nina kila kitu ninachohitaji.”+ Basi akaendelea kumsihi apokee zawadi hiyo, naye akaichukua.

12 Baadaye Esau akasema: “Tuondoke, tufunge safari, acha nikutangulie.” 13 Lakini Yakobo akamwambia: “Bwana wangu unajua kwamba watoto ni dhaifu+ nami nina kondoo na ng’ombe wanaonyonyesha. Wakipelekwa haraka-haraka kwa siku moja, wanyama wote watakufa. 14 Tafadhali, bwana wangu, nitangulie mimi mtumishi wako, lakini nitaendelea na safari polepole kulingana na mwendo wa mifugo na watoto mpaka nitakapofika kwako bwana wangu huko Seiri.”+ 15 Esau akasema: “Tafadhali, naomba niwaache baadhi ya watu wangu pamoja nawe.” Yakobo akasema, “Kwa nini ufanye hivyo? Naomba tu nipate kibali machoni pako, bwana wangu.” 16 Basi siku hiyo Esau akasafiri kurudi Seiri.

17 Naye Yakobo akaenda Sukothi,+ naye akajijengea nyumba na mabanda ya mifugo yake. Ndiyo sababu alipaita mahali hapo Sukothi.*

18 Baada ya kuondoka Padan-aramu,+ Yakobo akafika salama salimini kwenye jiji la Shekemu+ katika nchi ya Kanaani,+ naye akapiga kambi karibu na jiji hilo. 19 Kisha akanunua kisehemu fulani cha shamba kutoka kwa wana wa Hamori, baba ya Shekemu, kwa vipande 100 vya fedha, akapiga hema lake hapo.+ 20 Akajenga madhabahu huko na kuiita Mungu, Mungu wa Israeli.+

34 Sasa Dina, binti ya Yakobo na Lea,+ alizoea kwenda kuwatembelea* mabinti wengine nchini.+ 2 Shekemu mwana wa Hamori Mhivi,+ mkuu wa nchi, alipomwona, alimchukua na kumbaka. 3 Shekemu akavutiwa sana na Dina binti ya Yakobo, akampenda msichana huyo na kuanza kumtongoza.* 4 Hatimaye Shekemu akamwambia Hamori+ baba yake: “Nichukulie msichana huyu awe mke wangu.”

5 Yakobo aliposikia kwamba Shekemu alikuwa amembaka Dina binti yake, wanawe walikuwa na mifugo yake malishoni. Basi Yakobo akakaa kimya mpaka waliporudi. 6 Baadaye Hamori, baba ya Shekemu, akaja kuzungumza na Yakobo. 7 Lakini wana wa Yakobo wakasikia habari hizo, wakarudi haraka kutoka malishoni. Waliumia moyoni na kukasirika sana kwa sababu Shekemu alikuwa amemfedhehesha Israeli kwa kumbaka binti ya Yakobo,+ jambo ambalo halipaswi kufanywa.+

8 Hamori akazungumza nao, akisema: “Mwanangu Shekemu anamtamani sana* binti yenu. Tafadhali mpeni binti yenu awe mke wake, 9 na mfanye mapatano ya ndoa* pamoja nasi. Tupatieni mabinti wenu, nanyi mchukue mabinti wetu.+ 10 Mnaweza kuishi nasi na kukaa mahali popote nchini. Kaeni humu na kufanya biashara na kutulia nchini.” 11 Kisha Shekemu akamwambia baba ya Dina na ndugu zake: “Naomba nipate kibali machoni penu, nami nitawapa chochote mtakachoniomba. 12 Mnaweza kudai nitoe kiasi kikubwa sana cha mahari na zawadi.+ Niko tayari kuwapa chochote mtakachoniambia. Nipeni tu msichana huyu awe mke wangu.”

13 Wana wa Yakobo wakamjibu kwa hila Shekemu na Hamori baba yake, kwa sababu Shekemu alikuwa amembaka dada yao Dina. 14 Wakawaambia: “Hatuwezi kamwe kufanya jambo kama hilo, kukubali dada yetu aolewe na mwanamume ambaye hajatahiriwa,*+ kufanya hivyo ni fedheha kwetu. 15 Tunaweza kukubali tu kwa sharti hili: watahirini wanaume wenu wote, muwe kama sisi.+ 16 Ndipo tutakapowapa mabinti wetu na kuwachukua mabinti wenu, nasi tutaishi nanyi na kuwa familia moja. 17 Lakini msipotusikiliza na kutahiriwa, basi tutamchukua binti yetu na kwenda zetu.”

18 Maneno yao yakamfurahisha Hamori+ na Shekemu mwanawe.+ 19 Kijana huyo hakukawia kutimiza ombi lao,+ kwa sababu alimpenda binti ya Yakobo, naye Shekemu aliheshimiwa kuliko watu wote wa nyumba ya baba yake.

20 Kwa hiyo Hamori na Shekemu mwanawe wakaenda kwenye lango la jiji, wakazungumza na wanaume wa jiji lao+ wakisema: 21 “Wanaume hawa wangependa tuishi nao kwa amani. Waruhusuni wakae nchini na kufanya biashara humu, kwa maana nchi yetu ni kubwa vya kutosha. Tunaweza kuwaoa mabinti wao, nasi tunaweza kuwapa mabinti wetu.+ 22 Lakini watakubali tu kuishi nasi ili tuwe familia moja kwa sharti hili moja: kwamba kila mwanamume miongoni mwetu atahiriwe kama tu wanavyotahiriwa.+ 23 Tukifanya hivyo, je, mali zao, utajiri wao, na mifugo yao yote haitakuwa yetu? Basi acheni tutimize sharti lao ili waishi nasi.” 24 Wote waliokuwa wakitoka nje kupitia lango la jiji lake wakamsikiliza Hamori na Shekemu mwanawe, na wanaume wote wakatahiriwa, wote waliokuwa wakitoka nje kupitia lango la jiji.

25 Hata hivyo, siku ya tatu, walipokuwa bado wana maumivu, wana wawili wa Yakobo, Simeoni na Lawi, ndugu za Dina,+ wakachukua kila mmoja wao upanga wake, wakaenda ghafla katika jiji hilo na kumuua kila mwanamume.+ 26 Wakamuua Hamori na Shekemu mwanawe kwa upanga, kisha wakamchukua Dina kutoka katika nyumba ya Shekemu na kuondoka. 27 Wana wengine wa Yakobo walipofika waliona maiti za wanaume waliouawa, wakalipora jiji hilo kwa sababu dada yao alibakwa.+ 28 Wakachukua kondoo wao, mbuzi wao, ng’ombe wao, punda wao, na kitu chochote kilichokuwa jijini na shambani. 29 Walichukua pia mali zao zote, wakawachukua mateka wake zao na watoto wao wote, na kupora vitu vyote vilivyokuwa katika nyumba zao.

30 Basi Yakobo akawaambia Simeoni na Lawi:+ “Mmeniletea taabu kubwa* kwa kunifanya niwe uvundo kwa wakaaji wa nchi hii, Wakanaani na Waperizi. Nina watu wachache, nao kwa hakika wataungana na kunishambulia, nao wataniangamiza, mimi na nyumba yangu.” 31 Lakini wakamwambia: “Je, kuna yeyote anayepaswa kumtendea dada yetu kama kahaba?”

35 Baada ya hayo Mungu akamwambia Yakobo: “Ondoka, nenda Betheli+ ukaishi huko, na unijengee madhabahu mimi Mungu wa kweli, niliyekutokea ulipokuwa ukimkimbia ndugu yako Esau.”+

2 Basi Yakobo akawaambia watu wa nyumba yake na wote waliokuwa pamoja naye: “Ondoeni kabisa miungu ya kigeni iliyo kati yenu,+ na mjisafishe wenyewe na kubadili mavazi yenu, 3 na acheni tuondoke twende Betheli. Huko nitamjengea madhabahu Mungu wa kweli, aliyenijibu katika siku yangu ya taabu na ambaye amekuwa pamoja nami kila mahali nilipoenda.”*+ 4 Basi wakampa Yakobo miungu yote ya kigeni waliyokuwa nayo na vipuli walivyovaa masikioni, kisha Yakobo akavifukia* chini ya mti mkubwa uliokuwa karibu na Shekemu.

5 Walipokuwa wakisafiri, hofu ya Mungu iliyakumba majiji yaliyowazunguka, kwa hiyo wakaaji wake hawakuwafuatia wana wa Yakobo. 6 Hatimaye Yakobo akafika Luzi,+ yaani, Betheli, katika nchi ya Kanaani, pamoja na watu wote waliokuwa naye. 7 Akajenga madhabahu huko na kupaita mahali hapo El-betheli,* kwa sababu Mungu wa kweli alikuwa amemtokea mahali hapo alipomkimbia ndugu yake.+ 8 Baadaye Debora,+ mlezi wa Rebeka, akafa na kuzikwa chini ya mwaloni karibu na Betheli. Basi akauita mwaloni huo Alon-bakuthi.*

9 Mungu akamtokea Yakobo tena alipokuwa akitoka Padan-aramu, akambariki. 10 Mungu akamwambia: “Jina lako ni Yakobo.+ Hutaitwa tena Yakobo, jina lako litakuwa Israeli.” Naye akaanza kumwita Israeli.+ 11 Mungu akaendelea kumwambia: “Mimi ni Mungu Mweza-Yote.+ Zaa uwe na watoto wengi. Mataifa na kusanyiko la mataifa litatoka kwako,+ na wafalme watatoka kwako.*+ 12 Na nchi niliyompa Abrahamu na Isaka, nitakupa wewe na uzao wako* baada yako.”+ 13 Kisha Mungu akapanda na kumwacha mahali alipoongea naye.

14 Basi Yakobo akasimamisha nguzo mahali hapo alipoongea naye, nguzo ya mawe, naye akamimina toleo la kinywaji juu yake na pia akamimina mafuta juu yake.+ 15 Na Yakobo akaendelea kupaita mahali hapo ambapo Mungu alikuwa ameongea naye, Betheli.+

16 Kisha wakaondoka Betheli. Na walipokuwa umbali fulani kabla ya kufika Efrathi, Raheli akaanza kuzaa, na uchungu wa kuzaa ulikuwa mkali sana. 17 Lakini alipokuwa aking’ang’ana kuzaa, mkunga akamwambia: “Usiogope, kwa maana utamzaa mwana huyu pia.”+ 18 Uhai wake ulipokuwa ukitoka (kwa kuwa alikuwa akifa), akamwita mwana huyo Ben-oni,* lakini baba yake akamwita Benjamini.*+ 19 Kwa hiyo Raheli akafa na kuzikwa njiani kuelekea Efrathi, yaani, Bethlehemu.+ 20 Yakobo akasimamisha nguzo juu ya kaburi lake; hiyo ndiyo nguzo ya kaburi la Raheli mpaka leo hii.

21 Kisha Israeli akaendelea na safari na kupiga hema lake umbali fulani mbele ya mnara wa Ederi. 22 Siku moja, Israeli alipokuwa akiishi katika nchi hiyo, Rubeni alienda na kulala na Bilha suria wa baba yake, naye Israeli akasikia habari hizo.+

Basi Yakobo alikuwa na wana 12. 23 Wana wa Lea walikuwa Rubeni,+ mzaliwa wa kwanza wa Yakobo, kisha Simeoni, Lawi, Yuda, Isakari, na Zabuloni. 24 Wana wa Raheli walikuwa Yosefu na Benjamini. 25 Na wana wa Bilha kijakazi wa Raheli walikuwa Dani na Naftali. 26 Na wana wa Zilpa kijakazi wa Lea walikuwa Gadi na Asheri. Hao ndio wana wa Yakobo waliozaliwa Padan-aramu.

27 Hatimaye Yakobo akafika mahali ambapo Isaka baba yake alikuwa kule Mamre,+ Kiriath-arba, yaani, Hebroni, ambako Abrahamu na pia Isaka waliishi wakiwa wageni.+ 28 Isaka aliishi miaka 180.+ 29 Kisha Isaka akakata pumzi na kufa, akazikwa pamoja na watu wake,* baada ya kuishi maisha marefu na yenye kuridhisha;* na Esau na Yakobo wanawe wakamzika.+

36 Hii ndiyo historia ya Esau, yaani, Edomu.+

2 Esau alioa mabinti wa Kanaani: Ada+ binti ya Eloni Mhiti;+ na Oholibama+ binti ya Ana, mjukuu wa Sibeoni Mhivi; 3 na Basemathi,+ binti ya Ishmaeli, dada ya Nebayothi.+

4 Na Ada akamzalia Esau mtoto aliyeitwa Elifazi, naye Basemathi akamzaa Reueli,

5 na Oholibama akamzaa Yeushi, Yalamu, na Kora.+

Hao ndio wana wa Esau waliozaliwa katika nchi ya Kanaani. 6 Kisha Esau akawachukua wake zake, wanawe, mabinti zake, na watu wote wa nyumba yake, mifugo yake na wanyama wake wote, na mali yote aliyokusanya+ katika nchi ya Kanaani, akahamia nchi nyingine, umbali fulani kutoka kwa Yakobo ndugu yake.+ 7 Alihama kwa sababu mali zao zilikuwa nyingi sana wasiweze kuishi pamoja, na nchi walimoishi* haingewatosha kwa sababu walikuwa na mifugo mingi. 8 Kwa hiyo Esau akahamia eneo lenye milima la Seiri.+ Esau ndiye Edomu.+

9 Na hii ndiyo historia ya Esau, baba ya Waedomu walioishi katika eneo lenye milima la Seiri.+

10 Haya ndiyo majina ya wana wa Esau: Elifazi mwana wa Ada, mke wa Esau; Reueli mwana wa Basemathi, mke wa Esau.+

11 Wana wa Elifazi walikuwa Temani,+ Omari, Sefo, Gatamu, na Kenasi.+ 12 Timna akawa suria wa Elifazi, mwana wa Esau. Baada ya muda akamzalia Elifazi mtoto aliyeitwa Amaleki.+ Hao ndio wana wa Ada, mke wa Esau.

13 Hawa ndio wana wa Reueli: Nahathi, Zera, Shamma, na Miza. Hao ndio waliokuwa wana wa Basemathi,+ mke wa Esau.

14 Hawa ndio waliokuwa wana wa Oholibama binti ya Ana, mjukuu wa Sibeoni, mke wa Esau, aliomzalia Esau: Yeushi, Yalamu, na Kora.

15 Hawa ndio mashehe* wa wana wa Esau:+ Wana wa Elifazi, mzaliwa wa kwanza wa Esau: Shehe Temani, Shehe Omari, Shehe Sefo, Shehe Kenasi,+ 16 Shehe Kora, Shehe Gatamu, na Shehe Amaleki. Hao ndio mashehe wa Elifazi+ katika nchi ya Edomu. Hao ndio wana wa Ada.

17 Hawa ndio wana wa Reueli, mwana wa Esau: Shehe Nahathi, Shehe Zera, Shehe Shamma, na Shehe Miza. Hao ndio mashehe wa Reueli katika nchi ya Edomu.+ Hao ndio wana wa Basemathi, mke wa Esau.

18 Hatimaye hawa ndio wana wa Oholibama, mke wa Esau: Shehe Yeushi, Shehe Yalamu, na Shehe Kora. Hao ndio mashehe wa Oholibama binti ya Ana, mke wa Esau.

19 Hao ndio wana wa Esau, na hao ndio mashehe wao. Esau ndiye Edomu.+

20 Hawa ndio wana wa Seiri, Mhori, wakaaji wa nchi:+ Lotani, Shobali, Sibeoni, Ana,+ 21 Dishoni, Ezeri, na Dishani.+ Hao ndio mashehe wa Wahori, wana wa Seiri, katika nchi ya Edomu.

22 Wana wa Lotani walikuwa Hori na Hemamu, naye dada ya Lotani alikuwa Timna.+

23 Hawa ndio wana wa Shobali: Alvani, Manahathi, Ebali, Shefo, na Onamu.

24 Hawa ndio wana wa Sibeoni:+ Aya na Ana. Huyu ndiye Ana aliyepata chemchemi za maji ya moto nyikani alipokuwa akiwachunga punda wa Sibeoni baba yake.

25 Hawa ndio watoto wa Ana: Dishoni na Oholibama binti ya Ana.

26 Hawa ndio wana wa Dishoni: Hemdani, Eshbani, Ithrani, na Kerani.+

27 Hawa ndio wana wa Ezeri: Bilhani, Zaavani, na Akani.

28 Hawa ndio wana wa Dishani: Usi na Arani.+

29 Hawa ndio mashehe wa Wahori: Shehe Lotani, Shehe Shobali, Shehe Sibeoni, Shehe Ana, 30 Shehe Dishoni, Shehe Ezeri, na Shehe Dishani.+ Hao ndio mashehe wa Wahori, kila shehe katika nchi ya Seiri.

31 Sasa hawa ndio wafalme waliotawala katika nchi ya Edomu+ kabla mfalme yeyote hajawatawala Waisraeli.*+ 32 Bela mwana wa Beori alitawala Edomu, na jiji lake liliitwa Dinhaba. 33 Bela alipokufa, Yobabu mwana wa Zera kutoka Bosra akaanza kutawala baada yake. 34 Yobabu alipokufa, Hushamu kutoka katika nchi ya Watemani akaanza kutawala baada yake. 35 Hushamu alipokufa, Hadadi mwana wa Bedadi aliyewashinda Wamidiani+ katika eneo* la Moabu akaanza kutawala baada yake, na jiji lake liliitwa Avithi. 36 Hadadi alipokufa, Samla kutoka Masreka akaanza kutawala baada yake. 37 Samla alipokufa, Shauli kutoka Rehobothi karibu na ule Mto akaanza kutawala baada yake. 38 Shauli alipokufa, Baal-hanani mwana wa Akbori akaanza kutawala baada yake. 39 Baal-hanani mwana wa Akbori alipokufa, Hadari akaanza kutawala baada yake. Jiji lake liliitwa Pau, na mke wake aliitwa Mehetabeli binti ya Matredi binti ya Mezahabu.

40 Basi haya ndiyo majina ya mashehe wa Esau kulingana na koo zao, kulingana na maeneo yao, kulingana na majina yao: Shehe Timna, Shehe Alva, Shehe Yethethi,+ 41 Shehe Oholibama, Shehe Ela, Shehe Pinoni, 42 Shehe Kenasi, Shehe Temani, Shehe Mibsari, 43 Shehe Magdieli, na Shehe Iramu. Hao ndio mashehe wa Edomu kulingana na sehemu walizoishi katika nchi waliyomiliki.+ Hao ndio wazao wa Esau, baba ya Waedomu.+

37 Yakobo akaendelea kuishi katika nchi ya Kanaani, alikoishi baba yake akiwa mgeni.+

2 Hii ndiyo historia ya Yakobo.

Kijana Yosefu+ alipokuwa na umri wa miaka 17, alikuwa akichunga kondoo+ pamoja na wana wa Bilha+ na wana wa Zilpa,+ wake za baba yake. Naye Yosefu akamletea baba yake habari mbaya kuwahusu. 3 Sasa Israeli alimpenda sana Yosefu kuliko wanawe wengine+ kwa sababu alimzaa uzeeni, naye alikuwa amemshonea joho la pekee.* 4 Ndugu zake walipoona kwamba baba yao alimpenda sana kuliko yeyote miongoni mwao, wakaanza kumchukia, na hawakuzungumza naye kwa amani.

5 Baadaye Yosefu aliota ndoto na kuwasimulia ndugu zake,+ nao wakapata sababu zaidi ya kumchukia. 6 Aliwaambia hivi: “Tafadhali sikilizeni ndoto hii niliyoota. 7 Tulikuwa tukifunga matita ya masuke katikati ya shamba kisha tita langu likainuka na kusimama wima, nayo matita yenu yakalizunguka tita langu na kuliinamia.”+ 8 Ndugu zake wakamuuliza: “Je, kweli utajiweka kuwa mfalme wetu na kututawala?”+ Basi wakapata sababu nyingine ya kumchukia, kwa sababu ya ndoto zake na mambo aliyosema.

9 Baada ya hayo akaota tena ndoto nyingine, naye akawasimulia ndugu zake ndoto hiyo: “Nimeota ndoto nyingine. Wakati huu jua na mwezi na nyota 11 zilikuwa zikiniinamia.”+ 10 Kisha akamsimulia baba yake na ndugu zake ndoto hiyo, baba yake akamkemea na kumuuliza: “Ndoto hiyo yako inamaanisha nini? Je, kweli mimi na pia mama yako na ndugu zako tutakuja na kukuinamia mpaka ardhini?” 11 Basi ndugu zake wakazidi kumwonea wivu,+ lakini baba yake akayaweka akilini maneno yake.

12 Sasa ndugu zake wakaenda kulisha kondoo wa baba yao karibu na Shekemu.+ 13 Baadaye Israeli akamwambia Yosefu: “Ndugu zako wanachunga kondoo karibu na Shekemu, sivyo? Njoo nikutume kwao.” Yosefu akamwambia: “Niko tayari!” 14 Yakobo akamwambia: “Tafadhali, nenda uone kama ndugu zako wako salama. Angalia hali ya kondoo, uniletee habari.” Basi akamtuma kutoka katika bonde la* Hebroni,+ naye akashika njia kuelekea Shekemu. 15 Baadaye mtu fulani akamkuta akitangatanga mbugani. Mtu huyo akamuuliza: “Unatafuta nini?” 16 Akamjibu: “Ninawatafuta ndugu zangu. Tafadhali niambie, wanachunga kondoo wapi?” 17 Mtu huyo akamwambia: “Wameondoka hapa, niliwasikia wakisema, ‘Twendeni Dothani.’” Kwa hiyo Yosefu akawafuata ndugu zake na kuwakuta Dothani.

18 Sasa wakamwona akiwa mbali, na kabla hajafika karibu, wakaanza kupanga njama ya kumuua. 19 Wakaambiana: “Tazama! Ndiye yule mwota-ndoto anakuja.+ 20 Haya basi, njooni tumuue na kumtupa ndani ya shimo moja la maji, halafu tutasema kwamba aliliwa na mnyama mkali sana wa mwituni. Tuone itakuwaje kwa ndoto zake.” 21 Rubeni+ aliposikia maneno hayo, alijaribu kumwokoa ili wasimuue. Akasema: “Tusimuue.”+ 22 Kisha akawaambia: “Msimwage damu.+ Mtupeni ndani ya shimo hili la maji lililo nyikani, lakini msimdhuru.”*+ Rubeni alikusudia kumwokoa kutoka mikononi mwao ili amrudishe kwa baba yake.

23 Mara tu Yosefu alipowafikia ndugu zake, wakamvua joho lake la pekee,+ 24 kisha wakamchukua na kumtupa ndani ya shimo la maji. Wakati huo shimo hilo lilikuwa tupu; halikuwa na maji.

25 Kisha wakaketi chini ili wale chakula. Walipoinua macho yao, waliona msafara wa Waishmaeli+ ukija kutoka Gileadi. Ngamia wao walikuwa wamebeba gundi ya labdanamu, zeri, na magome yenye utomvu,+ nao walikuwa wakiteremka kwenda Misri. 26 Ndipo Yuda akawaambia ndugu zake: “Tutapata faida gani tukimuua ndugu yetu na kufunika damu yake?+ 27 Haya basi, acheni tumuuze+ kwa Waishmaeli, mkono wetu usimguse. Kwa kweli, yeye ni ndugu yetu na nyama yetu.” Kwa hiyo wakamsikiliza ndugu yao. 28 Basi wafanyabiashara hao Wamidiani+ walipokuwa wakipita, ndugu zake walimtoa shimoni na kumuuza kwa hao Waishmaeli kwa vipande 20 vya fedha.+ Watu hao wakampeleka Yosefu Misri.

29 Baadaye Rubeni aliporudi kwenye lile shimo la maji na kuona kwamba Yosefu hayumo shimoni, akayararua mavazi yake. 30 Aliporudi kwa ndugu zake, alisema kwa mshangao: “Mtoto amepotea! Sasa mimi—nitafanya nini?”

31 Basi wakalichukua joho la Yosefu, wakamchinja mbuzi dume na kulichovya joho hilo katika damu ya mbuzi huyo. 32 Kisha wakamtumia baba yao joho hilo na kumwambia: “Hiki ndicho tulichopata. Tafadhali chunguza uone ikiwa joho hili ni la mwanao au la.”+ 33 Basi akalichunguza na kusema kwa mshtuko: “Ni joho la mwanangu! Inaonekana ameliwa na mnyama mkali wa mwituni! Kwa hakika Yosefu ameraruliwa vipandevipande!” 34 Ndipo Yakobo akayararua mavazi yake na kuvaa nguo za magunia kiunoni na kumwombolezea mwanawe kwa siku nyingi. 35 Na wanawe wote na mabinti zake wote wakajaribu sana kumfariji, lakini alikataa kabisa kufarijiwa, akisema: “Nitashuka Kaburini*+ nikimwombolezea mwanangu!” Na baba yake akaendelea kumlilia.

36 Basi Wamidiani wakamuuza Yosefu Misri kwa Potifa, ofisa wa makao ya Farao+ aliyekuwa pia mkuu wa walinzi.+

38 Karibu wakati huo, Yuda aliwaacha ndugu zake na kupiga hema lake karibu na mwanamume Mwadulamu aliyeitwa Hira. 2 Akiwa huko, Yuda akamwona binti ya Mkanaani fulani+ aliyeitwa Shua. Basi akamwoa na kulala naye, 3 akapata mimba. Baadaye akazaa mwana, akampa jina Eri.+ 4 Akapata mimba tena, akazaa mwana na kumpa jina Onani. 5 Kwa mara nyingine tena akazaa mwana na kumpa jina Shela. Shela alipozaliwa, Yuda alikuwa Akzibu.+

6 Baada ya muda, Yuda akamtafutia Eri mzaliwa wake wa kwanza mke aliyeitwa Tamari.+ 7 Lakini Eri, mzaliwa wa kwanza wa Yuda, alimchukiza Yehova; kwa hiyo Yehova akamuua. 8 Kwa hiyo, Yuda akamwambia Onani: “Lala na mke wa ndugu yako na ufunge naye ndoa ya ndugu mkwe, umpe ndugu yako mzao.”+ 9 Lakini Onani alijua kwamba mzao huyo hangehesabiwa kuwa wake.+ Kwa hiyo alipolala na mke wa ndugu yake, alimwaga shahawa zake ardhini ili asimpe ndugu yake mzao.+ 10 Jambo alilofanya lilikuwa ovu machoni pa Yehova, kwa hiyo akamuua pia.+ 11 Yuda akamwambia Tamari binti mkwe wake: “Ishi ukiwa mjane katika nyumba ya baba yako mpaka Shela mwanangu atakapokua,” kwa maana Yuda alisema moyoni mwake: ‘Huenda yeye pia akafa kama ndugu zake.’+ Basi Tamari akaenda kuishi katika nyumba ya baba yake.

12 Muda fulani ukapita, na mke wa Yuda, aliyekuwa binti ya Shua,+ akafa. Yuda alizingatia kipindi cha maombolezo, kisha akaenda Timna+ kwa watumishi wake waliokata kondoo manyoya akiwa pamoja na rafiki yake, Hira, Mwadulamu.+ 13 Tamari akaambiwa: “Baba mkwe wako anapanda kwenda Timna kuwakata kondoo wake manyoya.” 14 Ndipo akayavua mavazi yake ya ujane, akajifunika uso kwa shela na kujifunika mabegani kwa mtandio, akaketi chini kwenye lango la kuingia Enaimu, jiji lililo katika barabara inayokwenda Timna, kwa sababu aliona kwamba Shela amekuwa mtu mzima lakini hajaruhusiwa amwoe.+

15 Yuda alipomwona, mara moja alifikiri yeye ni kahaba, kwa sababu alikuwa ameufunika uso wake. 16 Kwa hiyo, akamkaribia kando ya barabara na kumwambia: “Niruhusu tafadhali nilale nawe,” kwa maana hakujua kwamba alikuwa binti mkwe wake.+ Hata hivyo, Tamari akamuuliza: “Utanipa nini ili ulale nami?” 17 Akamjibu: “Nitakutumia mwanambuzi kutoka katika kundi langu.” Lakini akamuuliza: “Je, utanipa rehani kabla hujamleta?” 18 Yuda akamuuliza: “Ungependa nikupe nini kama rehani?” akasema: “Pete yako ya muhuri+ na kamba yako na fimbo uliyoshika mkononi.” Basi akampa vitu hivyo na kulala naye, Tamari akapata mimba. 19 Baada ya hayo Tamari akainuka na kwenda zake, akavua mtandio aliojifunika na kuvaa mavazi yake ya ujane.

20 Basi Yuda akamtuma rafiki yake Mwadulamu+ ampelekee mwanamke huyo mwanambuzi ili amrudishie vitu alivyompa kama rehani, lakini hakumpata kamwe. 21 Akawauliza watu wa jiji hilo: “Yuko wapi yule kahaba wa hekaluni anayekaa kando ya barabara hapa Enaimu?” Lakini wakamjibu: “Hatujawahi kumwona kahaba yeyote wa hekaluni mahali hapa.” 22 Mwishowe akarudi kwa Yuda na kumwambia: “Sikumpata, na isitoshe watu wa jiji hilo waliniambia, ‘Hatujawahi kumwona kahaba yeyote wa hekaluni mahali hapa.’” 23 Basi Yuda akasema: “Mwache avichukue vitu hivyo, tusije tukadharauliwa. Usijali, nilikutuma umpelekee mwanambuzi huyu, lakini hukumpata.”

24 Hata hivyo, baada ya miezi mitatu hivi, Yuda aliambiwa: “Tamari binti mkwe wako amefanya ukahaba, na pia amepata mimba kwa sababu ya ukahaba wake.” Yuda akasema: “Mtoeni nje achomwe moto.”+ 25 Alipokuwa akitolewa nje, akatuma ujumbe huu kwa baba mkwe wake: “Mwenye vitu hivi ndiye aliyenipa mimba.” Kisha akasema: “Tafadhali chunguza vitu hivi ni vya nani, yaani, pete hii ya muhuri na kamba na fimbo hii.”+ 26 Basi Yuda akavichunguza na kusema: “Yeye ni mwadilifu kuliko mimi, kwa sababu sikumruhusu Shela mwanangu amwoe.”+ Yuda hakufanya ngono naye tena baada ya hayo.

27 Wakati ulipofika wa Tamari kuzaa, mapacha walikuwa tumboni mwake. 28 Alipokuwa akizaa, mtoto mmoja alitoa mkono wake nje, na mara moja mkunga akachukua uzi mwekundu na kuufunga mkono huo, akisema: “Huyu alitoka kwanza.” 29 Lakini mara tu alipourudisha mkono wake, ndugu yake akatoka, mkunga akasema kwa mshangao: “Lo! Umejipasulia njia!” Basi akapewa jina Perezi.*+ 30 Kisha ndugu yake aliyefungwa uzi mwekundu mkononi akatoka, akapewa jina Zera.+

39 Basi Yosefu akapelekwa Misri,+ na Mmisri aliyeitwa Potifa,+ ofisa wa makao ya Farao aliyekuwa pia mkuu wa walinzi, akamnunua kutoka kwa Waishmaeli+ waliomleta huko. 2 Lakini Yehova alikuwa pamoja na Yosefu.+ Kwa hiyo akafanikiwa na kuwekwa kuwa msimamizi wa nyumba ya bwana wake, yule Mmisri. 3 Bwana wake akaona kwamba Yehova alikuwa pamoja naye na kwamba Yehova alikuwa akifanikisha kila jambo alilokuwa akifanya.

4 Yosefu akaendelea kupata kibali machoni pa Potifa, naye akawa mhudumu wake binafsi. Kwa hiyo Potifa akamweka kuwa msimamizi wa nyumba yake, na wa vitu vyake vyote. 5 Tangu alipomweka kuwa msimamizi wa nyumba yake na wa vitu vyake vyote, Yehova aliendelea kuibariki nyumba ya Mmisri huyo kwa sababu ya Yosefu, na Yehova akabariki vitu vyote alivyokuwa navyo nyumbani na shambani.+ 6 Hatimaye akamwachia Yosefu usimamizi wa vitu vyake vyote, naye hakujishughulisha na kitu chochote isipokuwa chakula chake. Isitoshe, Yosefu akawa mwanamume mwenye umbo zuri na sura inayopendeza.

7 Sasa baada ya hayo, mke wa bwana wake akaanza kumtupia jicho Yosefu na kumwambia: “Lala nami.” 8 Lakini akakataa na kumwambia mke wa bwana wake: “Tazama, bwana wangu hajui vitu nilivyo navyo nyumbani, naye ameniweka kuwa msimamizi wa vitu vyake vyote. 9 Hakuna yeyote aliye mkuu zaidi yangu katika nyumba hii, naye hajanikataza kitu chochote isipokuwa wewe, kwa sababu wewe ni mke wake. Basi ninawezaje kufanya uovu huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?”+

10 Basi siku baada ya siku alizungumza na Yosefu, lakini Yosefu hakukubali kamwe kulala naye wala kukaakaa naye. 11 Lakini siku moja kati ya siku ambazo Yosefu aliingia nyumbani kufanya kazi yake, hakukuwa na mtumishi yeyote nyumbani. 12 Basi mke wa Potifa akaishika kwa nguvu nguo ya Yosefu akisema: “Lala nami!” Lakini Yosefu akaiacha nguo yake mikononi mwake na kukimbilia nje. 13 Mara tu mke wa Potifa alipoona kwamba Yosefu ameiacha nguo yake mikononi mwake na kukimbilia nje, 14 akaanza kulia kwa sauti kubwa na kuwaita wanaume wa nyumbani mwake na kuwaambia: “Tazameni! Alituletea mwanamume huyu Mwebrania ili tuwe kichekesho. Alikuja kulala nami, lakini nikaanza kulia kwa sauti yangu yote. 15 Mara tu aliposikia nikilia kwa sauti kubwa na kupiga mayowe, akaiacha nguo yake kando yangu na kukimbilia nje.” 16 Kisha mke wa Potifa akaiweka nguo ya Yosefu kando yake mpaka bwana wake* aliporudi.

17 Halafu akamsimulia kisa hicho, akisema: “Yule mtumishi Mwebrania uliyetuletea alikuja kunifanya mimi niwe kichekesho. 18 Lakini mara tu nilipoanza kulia kwa sauti kubwa na kupiga mayowe, aliacha nguo yake kando yangu na kukimbilia nje.” 19 Punde tu bwana wa Yosefu alipomsikia mke wake akisema: “Hayo ndiyo mambo ambayo mtumishi wako alinitendea,” akawaka hasira. 20 Basi bwana wa Yosefu akamchukua Yosefu na kumtupa gerezani, mahali ambapo wafungwa wa mfalme walifungwa, akabaki humo gerezani.+

21 Lakini Yehova aliendelea kuwa pamoja na Yosefu, naye akazidi kumtendea kwa upendo mshikamanifu na kumfanya apate kibali machoni pa ofisa mkuu wa gereza.+ 22 Kwa hiyo, ofisa mkuu wa gereza akamweka Yosefu kuwa msimamizi wa wafungwa wote gerezani, na wa kazi zote walizokuwa wakifanya humo, yeye ndiye aliyehakikisha zimefanywa.+ 23 Ofisa mkuu wa gereza hakujishughulisha na jambo hata moja lililokuwa chini ya usimamizi wa Yosefu, kwa maana Yehova alikuwa pamoja na Yosefu na Yehova alifanikisha jambo lolote alilofanya.+

40 Baada ya hayo, msimamizi mkuu wa vinywaji+ na mwokaji mkuu wa mfalme wa Misri walimkosea bwana wao, mfalme wa Misri. 2 Kwa hiyo Farao akawakasirikia vikali maofisa hao wawili, msimamizi mkuu wa vinywaji na mwokaji mkuu,+ 3 akawatupa katika gereza lililokuwa katika nyumba ya mkuu wa walinzi,+ mahali ambapo Yosefu alikuwa amefungwa.+ 4 Kisha mkuu wa walinzi akamwagiza Yosefu akae nao na kuwatunza,+ nao wakakaa gerezani kwa muda fulani.*

5 Msimamizi wa vinywaji na mwokaji wa mfalme wa Misri, waliokuwa wamefungwa gerezani, waliota ndoto usiku mmoja, na kila ndoto ilikuwa na maana yake.* 6 Asubuhi iliyofuata, Yosefu alipoingia na kuwaona, walionekana wamehuzunika. 7 Basi akawauliza maofisa hao wa Farao waliokuwa naye gerezani katika nyumba ya bwana wake: “Mbona nyuso zenu zina huzuni leo?” 8 Wakamjibu: “Kila mmoja wetu aliota ndoto lakini hakuna mtu wa kutueleza maana yake.”* Yosefu akawaambia: “Je, si kazi ya Mungu kueleza maana ya ndoto?+ Tafadhali, nisimulieni ndoto zenu.”

9 Basi msimamizi mkuu wa vinywaji akamsimulia Yosefu ndoto yake akisema: “Katika ndoto yangu, niliona mzabibu mbele yangu. 10 Na mzabibu huo ulikuwa na matawi matatu, na ulipokuwa ukichipua vitawi, ulichanua maua, na zabibu zilizokuwa kwenye vishada vyake zikaiva. 11 Na kikombe cha Farao kilikuwa mikononi mwangu, nami nikachukua zabibu na kuzikamua ndani ya kikombe cha Farao. Kisha nikakiweka kikombe hicho mkononi mwa Farao.” 12 Ndipo Yosefu akamwambia: “Hii ndiyo maana yake. Yale matawi matatu ni siku tatu. 13 Siku tatu kuanzia leo, Farao atakutoa gerezani* na kukurudisha kwenye cheo chako,+ nawe utaendelea kuweka kikombe cha Farao mkononi mwake kama ulivyokuwa ukifanya ulipokuwa msimamizi wake wa vinywaji.+ 14 Hata hivyo, unikumbuke mambo yatakapokwendea vema. Tafadhali, nitendee kwa upendo mshikamanifu na umwambie Farao kunihusu, ili anitoe mahali hapa. 15 Ukweli ni kwamba nilitekwa nyara kutoka katika nchi ya Waebrania,+ nami sijafanya kosa lolote linalostahili nitupwe gerezani.”*+

16 Mwokaji mkuu alipoona kwamba Yosefu amesema* jambo jema kuhusu ndoto hiyo, akamwambia: “Mimi pia niliota ndoto, kulikuwa na vikapu vitatu vyenye mikate myeupe juu ya kichwa changu, 17 na katika kikapu cha juu, kulikuwa na kila aina ya vitu vilivyookwa kwa ajili ya Farao, na kulikuwa na ndege waliokula vitu vilivyokuwa katika kikapu kilichokuwa juu ya kichwa changu.” 18 Ndipo Yosefu akamwambia, “Hii ndiyo maana yake: Vile vikapu vitatu ni siku tatu. 19 Siku tatu kuanzia leo, Farao atakukata kichwa na kukutundika mtini, na ndege wataula mwili wako.”+

20 Sasa siku ya tatu ilikuwa sikukuu ya kuzaliwa kwa Farao,+ kwa hiyo aliwafanyia karamu watumishi wake wote, akamtoa gerezani msimamizi mkuu wa vinywaji na mwokaji mkuu, akawaleta mbele ya watumishi wake. 21 Akamrudisha msimamizi mkuu wa vinywaji kwenye cheo chake, akaendelea kumpa Farao kikombe. 22 Lakini akamtundika mwokaji mkuu, kama Yosefu alivyokuwa ameeleza.*+ 23 Hata hivyo, msimamizi mkuu wa vinywaji hakumkumbuka Yosefu; aliendelea kumsahau.+

41 Mwishoni mwa miaka miwili kamili, Farao aliota ndoto;+ katika ndoto hiyo alikuwa amesimama kando ya Mto Nile. 2 Na tazama! ng’ombe saba wazuri, walionona, walikuwa wakipanda kutoka mtoni, nao walikuwa wakila nyasi za Mto Nile.+ 3 Baada yao, ng’ombe wengine saba wenye sura mbaya na waliokonda walipanda kutoka katika Mto Nile, wakasimama karibu na wale ng’ombe wanono kwenye ukingo wa Mto Nile. 4 Kisha wale ng’ombe wenye sura mbaya, waliokonda, wakaanza kuwala wale ng’ombe saba wazuri, walionona. Ndipo Farao akaamka.

5 Kisha akarudi kulala, akaota ndoto ya pili. Kulikuwa na masuke saba ya nafaka yakitokea katika bua moja, yalikuwa yamejaa nafaka nayo yalikuwa mazuri sana.+ 6 Na baada ya hayo, masuke mengine saba ya nafaka yakakua, yalikuwa membamba na yalikuwa yamechomwa na upepo wa mashariki. 7 Kisha masuke hayo membamba ya nafaka yakaanza kuyameza yale masuke saba ya nafaka yaliyojaa nafaka na ambayo yalikuwa mazuri sana. Ndipo Farao akaamka na kugundua kwamba ilikuwa ndoto.

8 Lakini asubuhi, roho yake ikafadhaika. Basi akaagiza makuhani wote wachawi wa Misri na watu wake wote wenye hekima waitwe. Farao akawasimulia ndoto zake, lakini hakuna yeyote aliyeweza kumwambia Farao maana yake.*

9 Ndipo msimamizi mkuu wa vinywaji akamwambia Farao: “Ninaungama dhambi zangu leo. 10 Ee Farao, ulitukasirikia sisi watumishi wako. Kwa hiyo ukanifunga gerezani katika nyumba ya mkuu wa walinzi, mimi na mwokaji mkuu.+ 11 Kisha kila mmoja wetu akaota ndoto usiku uleule. Yeye na mimi, kila mmoja wetu aliota ndoto, na kila ndoto ilikuwa na maana yake.+ 12 Humo gerezani tulikuwa pamoja na kijana Mwebrania, mtumishi wa mkuu wa walinzi.+ Tulipomsimulia ndoto zetu,+ alitueleza maana ya kila ndoto. 13 Mambo yote yalitimia kama alivyotuambia.* Nilirudishwa katika cheo changu, lakini yule mwingine alitundikwa mtini.”+

14 Kwa hiyo Farao akaagiza Yosefu aletwe,+ basi wakamleta haraka kutoka gerezani.*+ Akajinyoa na kubadili nguo zake na kuingia mbele ya Farao. 15 Kisha Farao akamwambia Yosefu: “Niliota ndoto, lakini hakuna yeyote anayeweza kunieleza maana yake. Sasa nimesikia habari zako kwamba ukisimuliwa ndoto unaweza kueleza maana yake.”+ 16 Ndipo Yosefu akamjibu Farao: “Sistahili kusifiwa! Mungu ndiye atakayesema kuhusu hali yako, Ee Farao.”+

17 Farao akamwambia Yosefu: “Katika ndoto yangu, nilikuwa nimesimama kwenye ukingo wa Mto Nile. 18 Na tazama! ng’ombe saba wazuri, walionona, walikuwa wakipanda kutoka katika Mto Nile, wakaanza kula nyasi za Mto Nile.+ 19 Baada yao, ng’ombe wengine saba dhaifu, wenye sura mbaya sana, na waliokonda walipanda kutoka katika Mto Nile. Sijawahi kamwe kuona ng’ombe wenye sura mbaya hivyo katika nchi yote ya Misri. 20 Na ng’ombe hao waliokonda, wenye sura mbaya, wakaanza kuwala wale ng’ombe saba wa kwanza walionona. 21 Lakini baada ya kuwala, hakuna yeyote angejua kwamba wamewala ng’ombe hao, kwa kuwa sura yao ilikuwa mbaya kama mwanzoni. Ndipo nikaamka.

22 “Kisha nikaona katika ndoto yangu masuke saba ya nafaka yakitokea katika bua moja, yalikuwa yamejaa nafaka nayo yalikuwa mazuri sana.+ 23 Halafu yakafuatwa na masuke mengine saba ya nafaka yaliyonyauka, membamba, na yaliyochomwa na upepo wa mashariki. 24 Kisha yale masuke membamba ya nafaka yakaanza kuyameza yale masuke saba mazuri sana ya nafaka. Basi nikawasimulia makuhani wachawi ndoto hiyo,+ lakini hakuna yeyote aliyeweza kunieleza maana yake.”+

25 Ndipo Yosefu akamwambia Farao: “Ndoto zako ni ndoto moja, ndoto ileile. Mungu wa kweli amekuambia mambo atakayofanya.+ 26 Wale ng’ombe saba wazuri ni miaka saba. Na yale masuke saba mazuri ya nafaka ni miaka saba pia. Ndoto zako ni ndoto moja, ndoto ileile. 27 Wale ng’ombe saba waliokonda na wenye sura mbaya ambao walipanda baada ya wale wanono, ni miaka saba, na yale masuke saba ya nafaka yaliyo matupu, yaliyochomwa na upepo wa mashariki, yanamaanisha miaka saba ya njaa kali. 28 Hivi ndivyo nilivyokuambia, Ee Farao: Mungu wa kweli amekuonyesha mambo atakayofanya.

29 “Kutakuwa na miaka saba ya chakula kingi sana katika nchi yote ya Misri. 30 Lakini baada ya miaka hiyo, hakika kutakuwa na miaka saba ya njaa kali, nanyi hakika mtasahau chakula kingi sana kilichokuwa katika nchi ya Misri, na njaa hiyo kali itaiharibu nchi.+ 31 Nanyi hamtakumbuka chakula kingi sana kilichokuwa nchini kwa sababu ya njaa kali itakayofuata, kwa maana itakuwa kali sana. 32 Ee Farao, ulionyeshwa ndoto hiyo mara mbili kwa sababu Mungu wa kweli amekusudia kabisa jambo hilo, na Mungu wa kweli atalitimiza hivi karibuni.

33 “Sasa basi, Ee Farao, mtafute mwanamume mwenye busara na hekima umweke kuwa msimamizi wa nchi ya Misri. 34 Ee Farao, chukua hatua, waweke wasimamizi nchini, nawe utakusanya sehemu ya tano ya mazao yote nchini Misri katika miaka saba ya chakula kingi.+ 35 Nao wakusanye chakula chote katika miaka hiyo mizuri inayokuja, nao waweke nafaka katika maghala chini ya mamlaka yako Farao, na chakula hicho kihifadhiwe na kutunzwa katika majiji.+ 36 Chakula hicho kitaliwa nchini katika ile miaka saba ya njaa kali itakayoikumba nchi ya Misri, ili nchi isiangamie kwa sababu ya njaa hiyo kali.”+

37 Pendekezo hilo lilimfurahisha Farao na watumishi wake wote. 38 Kwa hiyo Farao akawaambia watumishi wake: “Je, kweli kuna mwanamume mwingine anayeweza kupatikana kama huyu aliye na roho ya Mungu?” 39 Kisha Farao akamwambia Yosefu: “Kwa kuwa Mungu amekuwezesha kuyajua yote hayo, hakuna yeyote aliye na busara na hekima kama wewe. 40 Wewe binafsi utaisimamia nyumba yangu, na watu wangu wote watakutii kabisa.+ Nitakuwa tu mkuu kuliko wewe ninapotimiza jukumu langu nikiwa mfalme.”* 41 Kisha Farao akamwambia Yosefu: “Tazama, ninakuweka kuwa msimamizi wa nchi yote ya Misri.”+ 42 Halafu Farao akaivua pete yake ya muhuri kutoka kwenye mkono wake mwenyewe na kumvisha Yosefu mkononi, akamvisha pia mavazi ya kitani bora na mkufu wa dhahabu shingoni mwake. 43 Zaidi ya hayo, akampandisha katika gari lake la pili la heshima, na watu walikuwa wakimtangulia na kusema kwa sauti, “Avrekh!”* Kwa hiyo Farao akamweka kuwa msimamizi wa nchi yote ya Misri.

44 Tena Farao akamwambia Yosefu: “Mimi ni Farao, lakini hakuna mtu anayepaswa kufanya jambo lolote* bila idhini yako katika nchi yote ya Misri.”+ 45 Kisha Farao akampa Yosefu jina Zafenath-panea, na pia akampa Asenathi+ binti ya Potifera kuhani wa Oni* awe mke wake. Naye Yosefu akaanza kuisimamia* nchi ya Misri.+ 46 Yosefu alikuwa na umri wa miaka 30+ alipoanza kumtumikia* Farao mfalme wa Misri.

Kisha Yosefu akaondoka mbele ya Farao na kutembea katika nchi yote ya Misri. 47 Na katika miaka saba ya chakula kingi, nchi ilizaa chakula kingi sana. 48 Naye aliendelea kukusanya chakula chote cha miaka saba katika nchi ya Misri, akakiweka katika maghala majijini. Katika kila jiji alikusanya chakula kutoka katika mashamba yaliyozunguka jiji hilo. 49 Yosefu akaendelea kukusanya nafaka nyingi sana katika maghala, kama mchanga wa bahari, hivi kwamba mwishowe wakaacha kuipima kwa sababu haingeweza kupimwa.

50 Kabla ya mwaka wa kwanza wa njaa kali, Asenathi, binti ya Potifera kuhani wa Oni* alimzalia Yosefu wana wawili.+ 51 Yosefu alimwita mzaliwa wa kwanza Manase,*+ kwa maana alisema, “Mungu amenifanya nisahau taabu yangu yote na nyumba yote ya baba yangu.” 52 Akamwita yule wa pili Efraimu,*+ kwa maana alisema, “Mungu ameniwezesha kuzaa watoto katika nchi ya mateso yangu.”+

53 Hatimaye miaka saba ya chakula kingi katika nchi ya Misri ikaisha,+ 54 na miaka saba ya njaa kali ikaanza, kama Yosefu alivyokuwa amesema.+ Njaa hiyo ilienea katika nchi zote, lakini kulikuwa na chakula* katika nchi yote ya Misri.+ 55 Mwishowe, nchi yote ya Misri ikakumbwa na njaa hiyo kali, watu wakaanza kumlilia Farao awape chakula.*+ Basi Farao akawaambia Wamisri wote: “Nendeni kwa Yosefu, na mfanye lolote atakalowaambia.”+ 56 Njaa hiyo ikaenea duniani pote.+ Ndipo Yosefu akaanza kuyafungua maghala yote ya nafaka yaliyokuwa katika majiji yao na kuwauzia Wamisri chakula,+ kwani njaa hiyo ilikuwa imeilemea sana nchi ya Misri. 57 Isitoshe, watu kutoka kila mahali duniani wakaja Misri kununua chakula kutoka kwa Yosefu, kwa sababu njaa hiyo ilikuwa imeilemea sana dunia yote.+

42 Yakobo aliposikia kwamba kuna nafaka nchini Misri,+ akawauliza wanawe: “Kwa nini mnatazamana tu?” 2 Kisha akawaambia: “Nimesikia kwamba kuna nafaka nchini Misri. Shukeni huko mkatununulie nafaka, ili tuendelee kuishi tusije tukafa.”+ 3 Basi ndugu kumi wa Yosefu+ wakashuka Misri kununua nafaka. 4 Lakini Yakobo hakumruhusu Benjamini,+ ndugu ya Yosefu, aende pamoja na ndugu zake, kwa sababu alisema: “Huenda akapatwa na madhara na kufa.”+

5 Kwa hiyo wana wa Israeli wakafika Misri pamoja na watu wengine walioenda kununua nafaka, kwa sababu njaa hiyo kali ilikuwa imeenea mpaka katika nchi ya Kanaani.+ 6 Yosefu ndiye aliyekuwa msimamizi nchini Misri,+ na ndiye aliyewauzia nafaka watu wote duniani.+ Kwa hiyo ndugu za Yosefu wakaja na kumwinamia kifudifudi.+ 7 Yosefu alipowaona ndugu zake, aliwatambua mara moja, lakini hakujitambulisha kwao.+ Basi akawauliza kwa ukali: “Mmetoka wapi?” wakamjibu: “Katika nchi ya Kanaani, tumekuja kununua chakula.”+

8 Basi Yosefu akawatambua ndugu zake, lakini wao hawakumtambua. 9 Mara moja Yosefu akakumbuka ndoto alizoota kuwahusu,+ akawaambia: “Ninyi ni wapelelezi! Mmekuja kuchunguza udhaifu wa nchi yetu!” 10 Wakamwambia: “Hapana, bwana wetu, sisi watumishi wako tumekuja kununua chakula. 11 Sisi sote ni wana wa mtu mmoja. Nasi ni wanyoofu. Sisi watumishi wako si wapelelezi.” 12 Lakini akawaambia: “Sivyo! Mmekuja kuchunguza udhaifu wa nchi yetu!” 13 Ndipo wakamwambia: “Sisi watumishi wako, ni ndugu 12.+ Sisi ni wana wa mtu mmoja+ anayeishi nchini Kanaani, na ndugu yetu mdogo amebaki na baba yetu,+ lakini mwingine hayupo tena.”+

14 Hata hivyo, Yosefu akawaambia: “Ni kama tu nilivyowaambia—‘Ninyi ni wapelelezi!’ 15 Hivi ndivyo mtakavyojaribiwa: Kwa hakika kama Farao anavyoishi, hamtatoka mahali hapa mpaka ndugu yenu mdogo atakapokuja.+ 16 Mtumeni mmoja wenu akamlete ndugu yenu, lakini ninyi wengine mtatiwa kifungoni. Kwa njia hiyo, maneno yenu yatajaribiwa ili ijulikane ikiwa mnasema ukweli. Na kama sivyo, basi, kwa hakika kama Farao anavyoishi, ninyi ni wapelelezi.” 17 Ndipo akawatia kifungoni kwa siku tatu.

18 Siku ya tatu, Yosefu akawaambia: “Fanyeni hili ili mwendelee kuishi, kwa sababu ninamwogopa Mungu. 19 Ikiwa ninyi ni wanyoofu, acheni ndugu yenu mmoja abaki katika nyumba ambamo mmefungiwa, lakini ninyi wengine mnaweza kwenda kuchukua nafaka ili mpunguze makali ya njaa katika nyumba zenu.+ 20 Kisha mleteni kwangu ndugu yenu mdogo, ili maneno yenu yathibitike kuwa ya kweli, nanyi hamtakufa.” Basi wakafanya hivyo.

21 Wakaambiana: “Bila shaka tunaadhibiwa kwa sababu ya ndugu yetu,+ kwa sababu tuliyaona mateso yake alipotusihi tumhurumie, lakini hatukumsikiliza. Ndiyo sababu tunateseka hivi.” 22 Kisha Rubeni akawaambia: “Je, sikuwaambia, ‘Msimdhuru mtoto,’* lakini hamkunisikiliza?+ Sasa kwa hakika tunadaiwa damu yake.”+ 23 Lakini hawakujua kwamba Yosefu alielewa mambo waliyokuwa wakisema, kwa sababu aliongea nao kupitia mkalimani. 24 Basi akaenda mbali nao na kuanza kulia.+ Aliporudi na kuzungumza nao, alimchukua Simeoni+ kutoka kati yao na kumfunga mbele ya macho yao.+ 25 Kisha Yosefu akaamuru mifuko yao ijazwe nafaka, na pesa za kila mmoja wao zirudishwe ndani ya gunia lake na pia wapewe vyakula kwa ajili ya safari. Ndivyo walivyofanyiwa.

26 Basi wakawatwika punda wao nafaka na kuondoka. 27 Walipofika mahali pa kulala, mmoja wao alifungua gunia lake ili amlishe punda wake, akaona pesa kwenye mdomo wa mfuko wake. 28 Akawaambia ndugu zake: “Pesa zangu zimerudishwa, ndizo hizi hapa kwenye mfuko wangu!” Wakashuka moyo, wakaanza kutetemeka na kuulizana: “Ni jambo gani hili ambalo Mungu ametutendea?”

29 Walipofika kwa Yakobo baba yao katika nchi ya Kanaani, wakamwambia mambo yote yaliyowapata, wakisema: 30 “Bwana mkubwa wa nchi hiyo alizungumza nasi kwa ukali+ na kudai kwamba tunaipeleleza nchi yao. 31 Lakini tukamwambia, ‘Sisi ni watu wanyoofu. Sisi si wapelelezi.+ 32 Sisi ni ndugu 12,+ wana wa baba mmoja. Mmoja wetu hayupo,+ na yule mdogo amebaki na baba yetu katika nchi ya Kanaani.’+ 33 Lakini bwana huyo akatuambia, ‘Hivi ndivyo nitakavyojua kwamba ninyi ni wanyoofu: Mwacheni ndugu yenu mmoja abaki nami.+ Kisha chukueni chakula mwende mkapunguze makali ya njaa ya watu wa nyumbani mwenu.+ 34 Mleteni kwangu ndugu yenu mdogo, ili nijue kwamba ninyi si wapelelezi bali ni watu wanyoofu. Kisha nitamrudisha ndugu yenu, nanyi mnaweza kufanya biashara katika nchi hii.’”

35 Walipokuwa wakimwaga nafaka kutoka katika magunia yao, kila mmoja wao alipata mfuko wake wa pesa katika gunia lake. Wote pamoja na baba yao walipoona mifuko yao ya pesa, wakaogopa. 36 Yakobo baba yao akashtuka na kusema: “Mmefanya nifiwe!+ Yosefu hayupo,+ Simeoni naye hayupo,+ na sasa mnataka kumchukua Benjamini! Mambo hayo yote yamenijia mimi!” 37 Lakini Rubeni akamwambia baba yake: “Unaweza kuwaua wanangu wawili nisipomrudisha kwako.+ Mweke chini ya uangalizi wangu, nami nitamrudisha kwako.”+ 38 Lakini Yakobo akasema: “Mwanangu hatashuka huko pamoja nanyi, kwa sababu ndugu yake amekufa, naye amebaki peke yake.+ Akipatwa na madhara na kufia njiani, basi kwa hakika mtazishusha mvi zangu Kaburini*+ kwa huzuni.”+

43 Sasa njaa ilikuwa kali sana nchini.+ 2 Basi walipomaliza kula nafaka waliyoleta kutoka Misri,+ baba yao akawaambia: “Rudini huko mkatununulie chakula kidogo.” 3 Yuda akamwambia: “Yule mtu alituonya waziwazi akisema, ‘Msiuone tena uso wangu msipokuja na ndugu yenu.’+ 4 Ukituruhusu twende na ndugu yetu, tutashuka huko na kukununulia chakula. 5 Lakini usipoturuhusu twende naye, hatutashuka kwenda huko, kwa sababu mtu huyo alituambia, ‘Msiuone uso wangu tena msipokuja na ndugu yenu.’”+ 6 Israeli+ akawauliza: “Kwa nini mmeniletea shida hii kwa kumwambia mtu huyo kwamba mna ndugu mwingine?” 7 Wakamjibu: “Mtu huyo alituuliza hivi moja kwa moja kutuhusu sisi na watu wetu wa ukoo: ‘Je, baba yenu angali hai? Je, mna ndugu mwingine?’ nasi tukamwambia ukweli.+ Tungejuaje atasema, ‘Mleteni ndugu yenu huku chini’?”+

8 Kisha Yuda akamsihi Israeli baba yake: “Niruhusu niende na mvulana huyu,+ acha twende zetu ili tuishi tusije tukafa+—wewe na sisi na watoto wetu.+ 9 Nitakuwa dhamana kwa ajili ya ulinzi wake.*+ Nitawajibika kwako. Nisipomrudisha na kukukabidhi, nitakuwa nimekutendea dhambi ya kudumu. 10 Lakini ikiwa hatungalikawia, kufikia sasa tungalikuwa tumefika huko na kurudi mara mbili.”

11 Kwa hiyo Israeli baba yao akawaambia: “Ikiwa ni lazima iwe hivyo, basi fanyeni hivi: Bebeni katika mifuko yenu vitu bora zaidi vya nchi yetu mkampelekee mtu huyo zawadi:+ zeri+ kidogo, asali kidogo, labdanamu, magome yenye utomvu,+ kungu, na lozi. 12 Bebeni kiasi maradufu cha pesa; na pia rudisheni pesa zilizowekwa kwenye midomo ya mifuko yenu.+ Huenda walikosea. 13 Mchukueni ndugu yenu mwende, rudini kwa mtu huyo. 14 Mungu Mweza-Yote na amchochee mtu huyo awahurumie, ili awaruhusu mrudi na yule ndugu yenu mwingine na Benjamini. Lakini ikiwa ni lazima nifiwe, basi nitafiwa!”+

15 Kwa hiyo wanaume hao wakachukua zawadi hiyo, kiasi maradufu cha pesa, na pia wakamchukua Benjamini. Wakaondoka na kushuka Misri, wakafika na kusimama tena mbele ya Yosefu.+ 16 Yosefu alipomwona Benjamini akiwa pamoja nao, mara moja akamwambia msimamizi wa nyumba yake: “Wapeleke watu hawa nyumbani, uchinje wanyama na kutayarisha chakula, kwa sababu watakula nami chakula cha mchana.” 17 Mara moja mtu huyo akafanya kama Yosefu alivyomwambia,+ akawapeleka nyumbani kwa Yosefu. 18 Lakini waliogopa walipopelekwa nyumbani kwa Yosefu, wakaanza kusema: “Tumeletwa hapa kwa sababu ya zile pesa zilizorudishwa katika mifuko yetu wakati uliopita. Sasa watatushambulia na kutufanya watumwa na kuchukua punda wetu!”+

19 Kwa hiyo wakamfikia msimamizi wa nyumba ya Yosefu, wakaongea naye kwenye mlango wa nyumba hiyo. 20 Wakamwambia: “Samahani, bwana wetu! Tulikuja huku chini mara ya kwanza kununua chakula.+ 21 Lakini tulipofika mahali tulipokuwa tukilala na kuanza kufungua mifuko yetu, tazama, kila mmoja wetu alikuta pesa zake kwenye mdomo wa mfuko wake, kiasi kilekile tulicholeta.+ Basi tungependa kuzirudisha sisi wenyewe. 22 Nasi tumeleta pesa zaidi za kununua chakula. Hatujui ni nani aliyeweka pesa zetu katika mifuko yetu.”+ 23 Msimamizi huyo akawaambia: “Ni sawa. Msiogope. Mungu wenu na Mungu wa baba yenu aliweka hazina katika mifuko yenu. Tayari nimepokea pesa zenu.” Baada ya hayo akamtoa Simeoni na kumleta kwao.+

24 Kisha msimamizi huyo akawapeleka ndani ya nyumba ya Yosefu, akawapa maji ya kunawa miguu na kuwapa punda wao chakula. 25 Nao wakatayarisha zawadi+ ya kumpa Yosefu atakapokuja mchana, kwa sababu walisikia kwamba wangekula chakula humo.+ 26 Yosefu alipoingia nyumbani, wakampelekea zawadi yao na kuinama kifudifudi mbele yake.+ 27 Kisha akawauliza kuhusu hali yao na kusema: “Baba yenu aliyezeeka mliyeniambia habari zake anaendeleaje? Je, angali hai?”+ 28 Wakamjibu: “Baba yetu ambaye ni mtumishi wako ni mzima. Angali hai.” Kisha wakainama chini na kuanguka kifudifudi.+

29 Alipoinua macho yake na kumwona Benjamini ndugu yake, mwana wa mama yake,+ akasema: “Je, huyu ndiye ndugu yenu mdogo mliyeniambia habari zake?”+ Kisha akamwambia: “Mungu na akupe kibali chake, mwanangu.” 30 Halafu Yosefu akatoka nje haraka kwa sababu alilemewa na hisia alipomwona ndugu yake, akatafuta mahali pa kulilia. Kwa hiyo akaingia katika chumba cha faragha na kulia huku akitokwa na machozi.+ 31 Kisha akanawa uso na kutoka chumbani, sasa akiwa amedhibiti hisia zake, akasema: “Leteni chakula.” 32 Basi wakampa Yosefu chakula chake na ndugu zake chakula chao, nao Wamisri waliokuwa pamoja naye wakala peke yao kwa sababu Wamisri hawangeweza kula pamoja na Waebrania, kwa sababu hilo ni jambo linalochukiza kwa Wamisri.+

33 Ndugu zake waliketi mbele yake, mzaliwa wa kwanza kulingana na haki yake ya mzaliwa wa kwanza+ na yule mdogo kulingana na umri wake, nao walikuwa wakitazamana kwa mshangao. 34 Yosefu alikuwa akiagiza chakula kichukuliwe kutoka kwenye meza yake na kupelekwa kwenye meza yao, lakini aliongeza chakula cha Benjamini mara tano zaidi ya chakula ambacho wengine wote walipewa.+ Basi wakaendelea kula na kunywa pamoja naye mpaka waliposhiba.

44 Baadaye Yosefu akamwamuru hivi msimamizi wa nyumba yake: “Ijaze mifuko ya watu hawa kiasi cha chakula wanachoweza kubeba, na uweke pesa za kila mmoja wao katika mdomo wa mfuko wake.+ 2 Lakini kiweke kile kikombe changu, kikombe changu cha fedha, katika mdomo wa mfuko wa yule mdogo, pamoja na pesa zake za nafaka.” Basi akafanya kama Yosefu alivyoagiza.

3 Asubuhi kulipopambazuka, wanaume hao waliruhusiwa kuondoka pamoja na punda wao. 4 Kabla hawajafika mbali kutoka jijini, Yosefu akamwambia yule msimamizi wa nyumba yake: “Ondoka! Wafuatie haraka wanaume hao! Utakapowafikia, waulize, ‘Kwa nini mmelipa uovu kwa wema? 5 Je, hiki si kikombe anachotumia bwana wangu kunywea na kukitumia kusoma kwa ustadi ishara za ubashiri? Jambo mlilotenda ni ovu.’”

6 Basi msimamizi huyo akawafikia na kuwaambia maneno hayo. 7 Lakini wakamwambia: “Kwa nini bwana wetu unasema jambo kama hili? Sisi watumishi wako hatuwezi kamwe kuwazia kufanya jambo lolote kama hilo. 8 Kwa kweli, pesa tulizopata kwenye midomo ya mifuko yetu tulikurudishia kutoka katika nchi ya Kanaani.+ Basi tungewezaje kuiba fedha au dhahabu katika nyumba ya bwana wako? 9 Yeyote kati ya watumwa wako atakayepatikana nacho, na auawe, na sisi wengine tutakuwa pia watumwa wa bwana wako.” 10 Kwa hiyo akasema: “Na iwe kama mlivyosema: Yule atakayepatikana nacho atakuwa mtumwa wangu, lakini ninyi wengine hamtakuwa na hatia.” 11 Basi kila mmoja akaushusha chini upesi mfuko wake na kuufungua. 12 Akaipekua mifuko hiyo kwa makini, akianza na mfuko wa yule mkubwa na kumalizia na mfuko wa yule mdogo. Hatimaye kikombe hicho kikapatikana katika mfuko wa Benjamini.+

13 Ndipo wakayararua mavazi yao, na kila mmoja akamtwika punda wake mfuko wake, wakarudi jijini. 14 Yuda+ na ndugu zake walipoingia katika nyumba ya Yosefu, bado alikuwemo; nao wakajiangusha chini mbele yake.+ 15 Yosefu akawauliza: “Ni jambo gani hili mlilofanya? Je, hamkujua kwamba mtu kama mimi anaweza kusoma kwa ustadi ishara za ubashiri?”+ 16 Yuda akamjibu: “Tukuambie nini bwana wetu? Tuseme nini? Tutathibitisha jinsi gani kwamba sisi ni waadilifu? Mungu wa kweli amefichua kosa letu sisi watumwa wako.+ Sasa sisi ni watumwa wako bwana wetu, sisi na yule aliyepatikana na kikombe hicho!” 17 Lakini akawaambia: “Siwezi kamwe kuwazia kufanya hivyo! Mtu aliyepatikana na kikombe hicho ndiye atakayekuwa mtumwa wangu.+ Lakini ninyi wengine, pandeni kwa amani mwende zenu kwa baba yenu.”

18 Sasa Yuda akamkaribia na kumwambia: “Nakusihi, bwana wangu, tafadhali niruhusu mimi mtumwa wako nikwambie neno moja bwana wangu, wala usinikasirikie mimi mtumwa wako, kwa maana wewe ni kama Farao.+ 19 Bwana wangu ulituuliza sisi watumwa wako, ‘Je, mna baba au ndugu?’ 20 Bwana wangu tukakuambia, ‘Tuna baba aliyezeeka na mtoto aliyemzaa uzeeni, yule mdogo.+ Lakini ndugu yake alikufa,+ kwa hiyo ndiye mwana pekee aliyebaki wa mama yake,+ na baba yake anampenda.’ 21 Kisha ukatuambia sisi watumwa wako, ‘Mleteni huku chini ili nimwone.’+ 22 Lakini bwana wangu tukakwambia, ‘Mvulana huyo hawezi kumwacha baba yake. Akimwacha, kwa hakika baba yake atakufa.’+ 23 Kisha ukatuambia sisi watumwa wako, ‘Ndugu yenu mdogo asiposhuka huku pamoja nanyi, hamtauona uso wangu tena.’+

24 “Basi tukapanda kwenda kwa mtumwa wako, baba yetu, na kumwambia maneno yako bwana wangu. 25 Baadaye baba yetu akatuambia, ‘Rudini huko mkatununulie chakula kidogo.’+ 26 Lakini tukamwambia, ‘Hatuwezi kushuka huko. Tutashuka ikiwa ndugu yetu mdogo atakuwa pamoja nasi, kwa sababu hatuwezi kuuona uso wa mtu huyo ndugu yetu mdogo asipokuwa pamoja nasi.’+ 27 Kisha mtumwa wako baba yetu akatuambia, ‘Mnajua vizuri kwamba mke wangu alinizalia wana wawili tu.+ 28 Lakini mmoja wao aliniacha, nikasema: “Kwa hakika mnyama wa mwituni amemrarua vipandevipande!”+ nami sijamwona mpaka sasa. 29 Mkimchukua huyu pia nisimwone, kisha apatwe na madhara na kufa, hakika mtazishusha mvi zangu Kaburini*+ kwa msiba.’+

30 “Na sasa nikirudi bila mvulana huyu kwa mtumwa wako baba yangu, kwa kuwa uhai wake umefungamana na uhai wa* mvulana huyu, 31 basi mara tu atakapoona mvulana huyu hayupo, atakufa, na kwa kweli sisi watumwa wako tutazishusha mvi za mtumwa wako baba yetu Kaburini* kwa huzuni. 32 Mimi mtumwa wako nilijitoa kuwa dhamana kwa baba yangu kwa ajili ya mvulana huyu, kwa kumwambia, ‘Nisipomrudisha kwako, nitakuwa nimekutendea dhambi milele baba yangu.’+ 33 Basi sasa tafadhali, acha niwe mtumwa wako bwana wangu badala ya mvulana huyu, ili arudi pamoja na ndugu zake. 34 Nitarudije kwa baba yangu bila mvulana huyu? Siwezi kustahimili kuona msiba huo ukimpata baba yangu!”

45 Ndipo Yosefu akashindwa kujizuia mbele ya watumishi wake wote.+ Basi akasema kwa sauti kubwa: “Mwondoeni kila mtu mbele yangu!” Hakuna yeyote aliyebaki pamoja na Yosefu alipokuwa akijitambulisha kwa ndugu zake.+

2 Kisha akaanza kulia kwa sauti kubwa hivi kwamba Wamisri wakamsikia na watu wa nyumba ya Farao wakamsikia. 3 Mwishowe Yosefu akawaambia ndugu zake: “Mimi ni Yosefu. Je, baba yangu angali hai?” Lakini ndugu zake wakashindwa kabisa kumjibu, kwa sababu walishtuka sana kusikia hivyo. 4 Basi Yosefu akawaambia ndugu zake: “Tafadhali, nikaribieni.” Basi wakamkaribia.

Kisha akawaambia: “Mimi ni Yosefu ndugu yenu, mliyemuuza Misri.+ 5 Lakini sasa msikasirike wala kulaumiana kwa kuniuza huku; kwa sababu Mungu alinituma huku niwatangulie ili kuokoa uhai.+ 6 Huu ni mwaka wa pili wa njaa kali nchini,+ na bado kuna miaka mitano ambayo watu hawataweza kulima wala kuvuna. 7 Lakini Mungu alinituma niwatangulie ili niwahifadhie ninyi wazao watakaobaki+ duniani* na ili mwendelee kuwa hai kupitia ukombozi mkubwa. 8 Hivyo basi, si ninyi mlionituma hapa, bali ni Mungu wa kweli, ili aniweke kuwa mshauri mkuu* wa Farao na msimamizi wa nyumba yake yote na mtawala wa nchi yote ya Misri.+

9 “Rudini upesi kwa baba yangu, mkamwambie, ‘Mwana wako Yosefu amesema hivi: “Mungu ameniweka kuwa msimamizi wa nchi yote ya Misri.+ Shuka uje kwangu. Usikawie.+ 10 Utaishi katika nchi ya Gosheni,+ utakuwa karibu nami—wewe, wana wako, wajukuu wako, makundi yako, mifugo yako, na kila kitu ulicho nacho. 11 Nitakupa chakula huko, kwa maana bado kuna miaka mitano ya njaa kali.+ La sivyo, utakuwa maskini, wewe na nyumba yako na kila kitu ulicho nacho.’” 12 Ninyi pamoja na ndugu yangu Benjamini mnajionea wenyewe kwamba kwa kweli ni mimi ninayezungumza nanyi.+ 13 Kwa hiyo mnapaswa kumwambia baba yangu kuhusu utukufu wangu wote nchini Misri na kila kitu mlichoona. Sasa fanyeni haraka mkamteremshe huku baba yangu.”

14 Kisha akamkumbatia* Benjamini ndugu yake na kuanza kulia, naye Benjamini akalia huku akiwa amemkumbatia shingoni.+ 15 Akawabusu ndugu zake wote na kuwalilia, kisha ndugu zake wakaongea naye.

16 Habari hizi zikafika katika nyumba ya Farao: “Ndugu za Yosefu wamekuja!” Habari hizo zikamfurahisha Farao na watumishi wake. 17 Basi Farao akamwambia Yosefu: “Waambie ndugu zako, ‘Fanyeni hivi: Watwikeni mizigo wanyama wenu wanaobeba mizigo, mwende katika nchi ya Kanaani, 18 mkamchukue baba yenu na familia zenu mje kwangu. Nitawapa vitu vizuri vya nchi ya Misri, nanyi mtakula* sehemu bora kabisa ya* nchi.+ 19 Nami nakuamuru uwaambie:+ ‘Fanyeni hivi: Chukueni magari ya kukokotwa+ kutoka katika nchi ya Misri ya kuwabeba watoto wenu na wake zenu, nanyi mnapaswa kutumia gari moja kumleta baba yenu.+ 20 Msijali kuhusu mali zenu,+ kwa sababu sehemu bora katika nchi yote ya Misri ni yenu.’”

21 Basi wana wa Israeli wakafanya hivyo, naye Yosefu akawapa magari ya kukokotwa kama Farao alivyoamuru, pia akawapa vyakula kwa ajili ya safari. 22 Akampa kila mmoja wao nguo ya kubadili, lakini akampa Benjamini vipande 300 vya fedha na nguo tano za kubadili.+ 23 Naye akamtumia baba yake vitu vifuatavyo: punda kumi waliobeba vitu vizuri vya Misri na punda majike kumi waliobeba nafaka na mikate na vyakula vingine kwa ajili ya safari yake. 24 Basi akawaaga ndugu zake, na walipokuwa wakiondoka akawaambia: “Msigombane njiani.”+

25 Basi wakapanda kutoka Misri na kufika katika nchi ya Kanaani kwa Yakobo baba yao. 26 Wakamwambia: “Yosefu angali hai, na ndiye mtawala wa nchi yote ya Misri!”+ Lakini moyo wake ukafa ganzi kwa sababu hakuwaamini.+ 27 Walipoendelea kumwambia mambo yote ambayo Yosefu aliwaambia na alipoona magari ya kukokotwa ambayo Yosefu aliwapa ili yambebe, roho ya Yakobo baba yao ikaanza kuhuika. 28 Israeli akasema kwa mshangao: “Inatosha! Yosefu mwanangu angali hai! Ni lazima niende kumwona kabla sijafa!”+

46 Basi Israeli akachukua kila kitu alichokuwa nacho* na kuondoka. Alipofika Beer-sheba,+ alimtolea dhabihu Mungu wa Isaka, baba yake.+ 2 Kisha Mungu akaongea na Israeli katika maono usiku na kumwambia: “Yakobo, Yakobo!” naye akajibu: “Mimi hapa!” 3 Akamwambia: “Mimi ndiye Mungu wa kweli, Mungu wa baba yako.+ Usiogope kushuka kwenda Misri, kwa maana huko nitakufanya uwe taifa kubwa.+ 4 Mimi mwenyewe nitashuka pamoja nawe Misri, na pia mimi mwenyewe nitakurudisha kutoka huko,+ na Yosefu atayafumba macho yako kwa mkono wake.”*+

5 Kisha Yakobo akaondoka Beer-sheba, na wanawe* wakamsafirisha Yakobo baba yao na watoto wao na wake zao katika magari ya kukokotwa ambayo Farao alikuwa amewapa ili yamsafirishe. 6 Wakachukua mifugo yao na mali zao, walizokuwa wamekusanya katika nchi ya Kanaani. Basi wakafika Misri, Yakobo na wazao wake wote. 7 Alienda Misri pamoja na wanawe na mabinti zake na wajukuu wake wa kiume na wa kike—wazao wake wote.

8 Sasa haya ndiyo majina ya wana wa Israeli waliokuja Misri,+ Yakobo na wanawe: mzaliwa wa kwanza wa Yakobo alikuwa Rubeni.+

9 Wana wa Rubeni walikuwa Hanoki, Palu, Hezroni, na Karmi.+

10 Wana wa Simeoni+ walikuwa Yemueli, Yamini, Ohadi, Yakini, Zohari, na Shauli+ mwana wa mwanamke Mkanaani.

11 Wana wa Lawi+ walikuwa Gershoni, Kohathi, na Merari.+

12 Wana wa Yuda+ walikuwa Eri, Onani, Shela,+ Perezi,+ na Zera.+ Lakini Eri na Onani walikufa katika nchi ya Kanaani.+

Wana wa Perezi walikuwa Hezroni na Hamuli.+

13 Wana wa Isakari walikuwa Tola, Puva, Iobu, na Shimroni.+

14 Wana wa Zabuloni+ walikuwa Seredi, Eloni, na Yahleeli.+

15 Hao ndio wana wa Lea, aliomzalia Yakobo huko Padan-aramu, kutia ndani Dina binti yake.+ Wanawe na mabinti zake wote walikuwa 33.

16 Wana wa Gadi+ walikuwa Zifioni, Hagi, Shuni, Esboni, Eri, Arodi, na Areli.+

17 Wana wa Asheri+ walikuwa Imna, Ishva, Ishvi, na Beria, na dada yao aliitwa Sera.

Wana wa Beria walikuwa Heberi na Malkieli.+

18 Hao ndio wana wa Zilpa,+ kijakazi ambaye Labani alimpa Lea binti yake. Alimzalia Yakobo wana hao: wote walikuwa 16.

19 Wana wa Raheli, mke wa Yakobo, walikuwa Yosefu+ na Benjamini.+

20 Katika nchi ya Misri, Asenathi+ binti ya Potifera kuhani wa Oni,* alimzalia Yosefu wana hawa: Manase+ na Efraimu.+

21 Wana wa Benjamini+ walikuwa Bela, Bekeri, Ashbeli, Gera,+ Naamani, Ehi, Roshi, Mupimu, Hupimu,+ na Ardi.+

22 Hao ndio wana ambao Raheli alimzalia Yakobo: wote walikuwa 14.

23 Mwana* wa Dani+ alikuwa Hushimu.+

24 Wana wa Naftali+ walikuwa Yahzeeli, Guni, Yezeri, na Shilemu.+

25 Hao ndio wana wa Bilha, kijakazi ambaye Labani alimpa Raheli binti yake. Alimzalia Yakobo wana hao: wote walikuwa saba.

26 Wazao wote wa Yakobo walioenda Misri pamoja naye walikuwa 66, bila kuhesabu wake wa wanawe.+ 27 Wana wa Yosefu aliowazaa akiwa Misri walikuwa wawili. Watu wote wa nyumba ya Yakobo waliokuja Misri walikuwa 70.+

28 Yakobo alimtuma Yuda+ atangulie na kumwambia Yosefu kwamba alikuwa njiani kwenda Gosheni. Walipofika katika nchi ya Gosheni,+ 29 Yosefu akaagiza gari lake litayarishwe, kisha akaenda kumpokea Israeli baba yake huko Gosheni. Alipokutana na baba yake, mara moja akamkumbatia* na kulia kwa muda.* 30 Kisha Israeli akamwambia Yosefu: “Sasa niko tayari kufa; nimeona uso wako na kujua kwamba ungali hai.”

31 Ndipo Yosefu akawaambia ndugu zake na watu wa nyumba ya baba yake: “Acheni nipande niende kumjulisha Farao,+ ‘Ndugu zangu na watu wa nyumba ya baba yangu waliokuwa katika nchi ya Kanaani wamekuja kwangu.+ 32 Watu hao ni wachungaji+ na wafugaji,+ nao wamekuja na kondoo wao na ng’ombe wao na kila kitu walicho nacho.’+ 33 Farao akiwaita na kuwauliza, ‘Mnafanya kazi gani?’ 34 Mnapaswa kumwambia, ‘Sisi watumishi wako tumekuwa wafugaji tangu tulipokuwa vijana mpaka sasa, sisi pamoja na mababu zetu,’+ ili mwishi katika nchi ya Gosheni,+ kwa sababu Wamisri wanamchukia kila mtu anayefuga kondoo.”+

47 Basi Yosefu akaenda na kumwambia Farao:+ “Baba yangu na ndugu zangu wamekuja kutoka katika nchi ya Kanaani wakiwa na kondoo wao na ng’ombe wao na mali zao zote, wako katika nchi ya Gosheni.”+ 2 Yosefu akachukua watano kati ya ndugu zake na kuwaleta mbele ya Farao.+

3 Farao akawauliza ndugu zake: “Mnafanya kazi gani?” Wakamjibu: “Sisi watumishi wako ni wafugaji wa kondoo, sisi na mababu zetu.”+ 4 Kisha wakamwambia Farao: “Sisi watumishi wako tumekuja kuishi nchini kama wageni+ kwa sababu hakuna malisho kwa ajili ya mifugo yetu, kwa kuwa njaa ni kali sana katika nchi ya Kanaani.+ Basi tafadhali turuhusu sisi watumishi wako tuishi katika nchi ya Gosheni.”+ 5 Ndipo Farao akamwambia Yosefu: “Baba yako na ndugu zako wamekuja hapa kwako. 6 Nchi ya Misri iko mbele yako. Wape baba yako na ndugu zako sehemu bora kabisa ya nchi+ ili waishi humo. Waache waishi katika nchi ya Gosheni, na ikiwa unajua wanaume wowote wenye ustadi miongoni mwao, waweke wasimamie mifugo yangu.”

7 Kisha Yosefu akamleta Yakobo baba yake na kumpeleka mbele ya Farao, naye Yakobo akambariki Farao. 8 Farao akamuuliza Yakobo: “Una umri gani?” 9 Yakobo akamwambia Farao: “Nimekuwa nikitangatanga* kwa miaka 130. Miaka yangu imekuwa michache na yenye taabu,+ nayo si mingi kama miaka ambayo mababu zangu waliishi walipokuwa wakitangatanga.”*+ 10 Kisha Yakobo akambariki Farao na kutoka mbele yake.

11 Basi Yosefu akawapa makao baba yake na ndugu zake, aliwapa miliki katika nchi ya Misri, katika sehemu bora kabisa ya nchi, katika eneo la Ramesesi,+ kama Farao alivyoamuru. 12 Na Yosefu akaendelea kumpa chakula* baba yake na ndugu zake na watu wote wa nyumba ya baba yake, kulingana na idadi ya watoto wao.

13 Sasa nchi yote haikuwa na chakula* kwa sababu njaa ilikuwa kali sana, basi watu wakadhoofika katika nchi ya Misri na nchi ya Kanaani kwa sababu ya njaa hiyo.+ 14 Yosefu alikuwa akikusanya pesa zote katika nchi ya Misri na nchi ya Kanaani, pesa za nafaka iliyonunuliwa na watu,+ naye alikuwa akizipeleka katika nyumba ya Farao. 15 Hatimaye watu wa nchi ya Misri na nchi ya Kanaani wakaishiwa na pesa, na Wamisri wote wakaanza kwenda kwa Yosefu na kumwambia: “Tupe chakula! Kwa nini tufe ukituangalia kwa kuwa pesa zetu zimekwisha?” 16 Yosefu akawaambia: “Ikiwa pesa zenu zimekwisha, leteni mifugo yenu, nami nitawapa chakula na kuchukua mifugo yenu.” 17 Basi wakaanza kumletea Yosefu mifugo yao, naye alikuwa akiwapa chakula na kuchukua farasi wao, mifugo yao, na punda wao, na mwaka huo wote alikuwa akiwapa chakula na kuchukua mifugo yao yote.

18 Mwaka huo ulipokwisha, walianza kumjia mwaka uliofuata wakisema: “Hatutakuficha bwana wetu kwamba tumekupa pesa zetu zote na mifugo yetu yote. Hatuna chochote kilichobaki cha kukupa bwana wetu isipokuwa miili yetu na ardhi yetu. 19 Kwa nini tufe ukituangalia, sisi na ardhi yetu? Tununue sisi pamoja na ardhi yetu tupate chakula, nasi pamoja na ardhi yetu tutakuwa watumwa wa Farao. Tupe mbegu ili tuendelee kuishi, tusife, na ardhi yetu isibaki ukiwa.” 20 Basi Yosefu akamnunulia Farao ardhi yote ya Wamisri, kwa sababu kila Mmisri aliuza ardhi yake, kwa maana njaa ilikuwa kali sana; ardhi ikawa mali ya Farao.

21 Kisha akawahamisha watu na kuwapeleka majijini, kutoka mwisho mmoja wa nchi ya Misri mpaka mwisho mwingine.+ 22 Ila tu hakununua ardhi ya makuhani,+ kwa sababu makuhani walipata posho ya chakula kutoka kwa Farao, nao waliishi kwa kutegemea posho waliyopewa na Farao. Ndiyo sababu hawakuuza ardhi yao. 23 Kisha Yosefu akawaambia watu: “Tazameni, leo nimewanunua ninyi na ardhi yenu kuwa mali ya Farao. Hapa pana mbegu kwa ajili yenu, zipandeni mashambani. 24 Mtakapopata mavuno, mpeni Farao sehemu ya tano ya mavuno hayo,+ lakini sehemu nne zitakuwa zenu; zitakuwa mbegu za kupanda shambani na chakula chenu na cha watu wa nyumbani mwenu na cha watoto wenu.” 25 Basi wakamwambia: “Umeokoa uhai wetu.+ Na tupate kibali machoni pako bwana wetu, nasi tutakuwa watumwa wa Farao.”+ 26 Kisha Yosefu akaifanya hiyo kuwa sheria ambayo ingali inafanya kazi nchini Misri hadi leo, kwamba sehemu ya tano ya mavuno ni ya Farao. Ni ardhi ya makuhani tu ambayo haikununuliwa na Farao.+

27 Waisraeli wakaendelea kuishi Misri, katika nchi ya Gosheni,+ wakakaa humo, nao wakaongezeka na kuwa wengi sana.+ 28 Na Yakobo akaendelea kuishi katika nchi ya Misri kwa miaka 17, kwa hiyo siku zote za maisha ya Yakobo zilikuwa miaka 147.+

29 Wakati wa Israeli kufa ulikuwa ukikaribia,+ kwa hiyo akamwita Yosefu mwanawe na kumwambia: “Ikiwa sasa nimepata kibali machoni pako, tafadhali, weka mkono wako chini ya paja langu, na unitendee kwa upendo mshikamanifu na uaminifu. Tafadhali, usinizike Misri.+ 30 Nitakapokufa,* unapaswa kunibeba na kunitoa Misri na kunizika katika kaburi la mababu zangu.”+ Basi Yosefu akasema: “Nitafanya tu kama unavyosema.” 31 Kisha Yakobo akasema: “Niapie.” Basi akamwapia.+ Ndipo Israeli akainama upande wa kichwa cha kitanda chake.+

48 Baada ya hayo, Yosefu akaambiwa: “Tazama, baba yako anadhoofika.” Basi akawachukua wanawe wawili, Manase na Efraimu, na kwenda nao.+ 2 Ndipo Yakobo akaambiwa: “Tazama, mwana wako Yosefu amekuja kukuona.” Basi Israeli akajikakamua na kuketi kitandani. 3 Yakobo akamwambia Yosefu:

“Mungu Mweza-Yote alinitokea kule Luzi katika nchi ya Kanaani na kunibariki.+ 4 Naye akaniambia, ‘Ninakufanya uzae, nami nitakufanya uwe na watoto wengi, nami nitakufanya uwe kusanyiko la mataifa,+ nami nitaupa uzao wako* baada yako nchi hii iwe miliki yao ya kudumu.’+ 5 Sasa wana wako wawili uliowazaa katika nchi ya Misri kabla sijaja kwako nchini Misri ni wangu.+ Efraimu na Manase watakuwa wangu kama Rubeni na Simeoni walivyo wangu.+ 6 Lakini watoto utakaowazaa baada yao watakuwa wako. Wataitwa kwa jina la ndugu zao katika urithi wao.+ 7 Nilipokuwa nikitoka Padani, Raheli alikufa+ kando yangu katika nchi ya Kanaani, na bado tulikuwa na safari ndefu kabla ya kufika Efrathi.+ Kwa hiyo nikamzika huko nikiwa njiani kuelekea Efrathi, yaani, Bethlehemu.”+

8 Kisha Israeli akawaona wana wa Yosefu na kuuliza: “Ni nani hawa?” 9 Yosefu akamwambia baba yake: “Hawa ni wanangu ambao Mungu amenipa mahali hapa.”+ Yakobo akasema: “Tafadhali walete karibu nami ili niwabariki.”+ 10 Sasa macho ya Israeli yalikuwa yamedhoofika kwa sababu ya uzee, naye hangeweza kuona. Basi Yosefu akawaleta karibu naye, Yakobo akawabusu na kuwakumbatia. 11 Israeli akamwambia Yosefu: “Sikuwazia kamwe kwamba nitauona uso wako,+ lakini sasa Mungu ameniruhusu pia kuona uzao wako.”* 12 Kisha Yosefu akawaondoa kwenye magoti ya Israeli, naye akainama kifudifudi.

13 Halafu Yosefu akawachukua wote wawili na kuwaleta karibu na Yakobo; alimchukua Efraimu+ kwa mkono wake wa kulia na kumweka upande wa kushoto wa Israeli, na Manase+ kwa mkono wake wa kushoto na kumweka upande wa kulia wa Israeli. 14 Lakini Israeli akaunyoosha mkono wake wa kulia na kuuweka juu ya kichwa cha Efraimu, ingawa ndiye aliyekuwa mdogo, halafu akauweka mkono wake wa kushoto juu ya kichwa cha Manase. Aliweka mikono yake hivyo kimakusudi kwa sababu Manase alikuwa mzaliwa wa kwanza.+ 15 Kisha akambariki Yosefu na kusema:+

“Mungu wa kweli ambaye baba zangu Isaka na Abrahamu walitembea mbele zake,+

Mungu wa kweli ambaye amekuwa akinichunga maisha yangu yote mpaka leo,+

16 Malaika ambaye amekuwa akiniponya katika misiba yote,+ awabariki wavulana hawa.+

Na waitwe kwa jina langu na jina la baba zangu, Abrahamu na Isaka,

Acha waongezeke na kuwa umati mkubwa duniani.”+

17 Yosefu hakufurahi alipoona baba yake ameuweka mkono wake wa kulia juu ya kichwa cha Efraimu, basi akashika mkono wa baba yake na kujaribu kuuondoa juu ya kichwa cha Efraimu ili auweke juu ya kichwa cha Manase. 18 Yosefu akamwambia baba yake: “Sivyo baba yangu, kwa kuwa huyu ndiye mzaliwa wa kwanza.+ Weka mkono wako wa kulia juu ya kichwa chake.” 19 Lakini baba yake akazidi kukataa na kusema: “Najua, mwanangu, najua. Yeye pia atakuwa taifa, yeye pia atakuwa mkuu. Hata hivyo, ndugu yake mdogo atakuwa mkuu kuliko yeye,+ na uzao wake utalingana* kabisa na mataifa.”+ 20 Basi akaendelea kuwabariki siku hiyo,+ akisema:

“Waisraeli na walitaje jina lenu wanapotangaza baraka, wakisema,

‘Mungu na awafanye muwe kama Efraimu na kama Manase.’”

Hivyo akaendelea kumtanguliza Efraimu mbele ya Manase.

21 Kisha Israeli akamwambia Yosefu: “Tazama, ninakufa, + lakini kwa hakika Mungu ataendelea kuwa pamoja nanyi na kuwarudisha katika nchi ya mababu zenu.+ 22 Mimi ninakupa sehemu moja zaidi ya nchi* kuliko ndugu zako, ambayo nilichukua kutoka mikononi mwa Waamori kwa upanga wangu na upinde wangu.”

49 Basi Yakobo akawaita wanawe na kuwaambia: “Kusanyikeni pamoja niwaambie yatakayowapata katika kipindi cha mwisho cha zile siku. 2 Kusanyikeni msikilize, enyi wana wa Yakobo, naam, msikilizeni Israeli baba yenu.

3 “Rubeni,+ wewe ndiye mzaliwa wangu wa kwanza,+ nguvu zangu na mwanzo wa nguvu zangu za uzazi, ubora wa heshima na ubora wa nguvu. 4 Kwa vurugu kama maji yenye msukosuko, hutafanikiwa, kwa sababu ulikipanda kitanda cha baba yako.+ Wakati huo ulikichafua* kitanda changu. Kwa kweli alikipanda kitanda changu!

5 “Simeoni na Lawi ni ndugu.+ Silaha za ukatili ndizo silaha zao za kuchinjia.+ 6 Usijiunge nao, Ee nafsi* yangu. Usijiunge na kusanyiko lao, Ee heshima yangu,* kwa sababu kwa hasira yao waliwaua wanaume,+ nao wakawakata ng’ombe dume mishipa ya miguu ili kujifurahisha. 7 Na ilaaniwe hasira yao, kwa sababu ni katili, na ghadhabu yao, kwa sababu ni kali.+ Acheni niwatawanye katika Yakobo, na acheni niwasambaze katika Israeli.+

8 “Nawe Yuda,+ ndugu zako watakusifu.+ Mkono wako utakuwa shingoni mwa maadui wako.+ Wana wa baba yako watainama chini mbele yako.+ 9 Yuda ni mwanasimba.+ Mwanangu, kwa hakika utapanda juu kutoka mawindoni. Amejikunyata chini na kujinyoosha kama simba, na kama simba, ni nani anayethubutu kumwamsha? 10 Fimbo ya ufalme haitaondoka Yuda,+ wala fimbo ya kiongozi kutoka katikati ya miguu yake, mpaka Shilo* atakapokuja,+ na mataifa yatamtii.+ 11 Atamfunga punda wake kwenye mzabibu na mwanapunda dume wake kwenye mzabibu bora, naye atafua nguo zake katika divai na vazi lake katika damu ya zabibu. 12 Macho yake ni mekundu sana kwa sababu ya divai, na meno yake ni meupe kwa sababu ya maziwa.

13 “Zabuloni+ atakaa kwenye ufuo wa bahari, kwenye ufuo ambapo meli hutia nanga,+ na mpaka wake wa mbali utaelekea Sidoni.+

14 “Isakari+ ni punda mwenye mifupa migumu, aliyelala chini kati ya mizigo miwili aliyobeba. 15 Naye ataona kwamba mahali pa kupumzikia ni pazuri na kwamba nchi inapendeza. Atainamisha bega lake ili abebe mzigo, naye atakubali kufanya kazi ya utumwa.

16 “Dani+ atawahukumu watu wake akiwa mmoja wa makabila ya Israeli.+ 17 Dani na awe nyoka kando ya barabara, nyoka mwenye pembe kando ya njia, anayeuma visigino vya farasi na kumwangusha nyuma mpandaji wake.+ 18 Nitasubiri wokovu kutoka kwako, Ee Yehova.

19 “Naye Gadi+ atavamiwa na kundi la wavamizi, lakini atawavamia kwenye visigino vyao.+

20 “Mkate wa Asheri+ utakuwa mwingi sana,* naye ataandaa chakula kinachomfaa mfalme.+

21 “Naftali+ ni paa jike mwembamba. Anasema maneno yanayovutia sana.+

22 “Yosefu+ ni chipukizi la mti unaozaa matunda mengi, mti ulio kando ya chemchemi unaozaa matunda mengi, wenye matawi yanayoenea juu ya ukuta. 23 Lakini wapiga mishale waliendelea kumshambulia na kumpiga kwa mishale na kuendelea kuwa na uadui dhidi yake.+ 24 Lakini bado upinde wake ulibaki mahali pake,+ na mikono yake ikaendelea kuwa na nguvu na myepesi.+ Alitiwa nguvu na mikono ya mwenye nguvu wa Yakobo, mchungaji, jiwe la Israeli. 25 Anatoka* kwa Mungu wa baba yako, naye atakusaidia, naye yuko pamoja na Mweza-Yote, atakubariki kwa baraka za mbingu zilizo juu, kwa baraka za vilindi vilivyo chini,+ kwa baraka za matiti na tumbo la uzazi. 26 Baraka za baba yako zitakuwa bora kuliko baraka za milima ya milele, bora kuliko vitu vyenye kutamanika vya vilima vinavyodumu.+ Zitaendelea kuwa juu ya kichwa cha Yosefu, juu ya utosi wa kichwa cha yule aliyechaguliwa kutoka kati ya ndugu zake.+

27 “Benjamini+ ataendelea kurarua kama mbwamwitu.+ Asubuhi atakula mawindo, na jioni atagawanya nyara.”+

28 Hayo yote ndiyo makabila 12 ya Israeli, na hivyo ndivyo baba yao alivyowaambia alipokuwa akiwabariki. Alimpa kila mmoja wao baraka inayomfaa.+

29 Baada ya hayo aliwapa maagizo haya: “Nakaribia kufa.*+ Nizikeni pamoja na baba zangu katika pango lililo kwenye shamba la Efroni Mhiti,+ 30 pango lililo katika shamba la Makpela mbele ya Mamre katika nchi ya Kanaani, shamba ambalo Abrahamu alinunua kutoka kwa Efroni Mhiti ili liwe mahali pa kuzikia. 31 Walimzika huko Abrahamu na Sara mke wake.+ Walimzika huko Isaka+ na Rebeka mke wake, na huko ndiko nilikomzika Lea. 32 Shamba hilo na pango lililomo lilinunuliwa kutoka kwa wana wa Hethi.”+

33 Basi Yakobo akamaliza kuwapa wanawe maagizo hayo. Kisha akairudisha miguu yake kitandani, akakata pumzi, naye akazikwa pamoja na watu wake.*+

50 Ndipo Yosefu akamwangukia baba yake,+ akamlilia na kumbusu. 2 Kisha Yosefu akawaamuru watumishi wake, matabibu, wampake baba yake dawa ili asioze. + Basi matabibu hao wakampaka dawa Israeli, 3 wakafanya hivyo kwa siku 40, muda kamili uliotumiwa kupaka dawa, nao Wamisri wakaendelea kumlilia kwa siku 70.

4 Siku za kumwombolezea zilipopita, Yosefu akawaambia hivi watu wa makao* ya Farao: “Ikiwa nimepata kibali machoni penu, mpeni Farao ujumbe huu: 5 ‘Baba yangu aliniapisha+ akisema: “Tazama! ninakufa.+ Nizike katika kaburi langu+ nililochimba katika nchi ya Kanaani.”+ Tafadhali, niruhusu nipande kwenda kumzika baba yangu, kisha nitarudi.’” 6 Farao akajibu: “Nenda ukamzike baba yako kama alivyokuapisha.”+

7 Basi Yosefu akapanda kwenda kumzika baba yake, alienda pamoja na watumishi wote wa Farao, wazee+ wa makao ya Farao na wazee wote wa nchi ya Misri 8 na watu wote wa nyumba ya Yosefu na ndugu zake na watu wa nyumba ya baba yake.+ Watoto wao wadogo na kondoo wao na ng’ombe wao ndio tu waliobaki katika nchi ya Gosheni. 9 Alienda pia na magari+ na wapanda farasi; lilikuwa kundi kubwa sana. 10 Kisha wakafika kwenye uwanja wa kupuria wa Atadi, katika eneo la Yordani, na huko wakafanya maombolezo makubwa sana na kulia kwa uchungu, naye akaendelea kumwombolezea baba yake kwa siku saba. 11 Wakaaji wa nchi, Wakanaani, wakawaona wakiomboleza kwenye uwanja wa kupuria wa Atadi, wakasema kwa mshangao: “Haya ni maombolezo makubwa sana ya Wamisri!” Ndiyo sababu mahali hapo paliitwa Abel-misraimu,* katika eneo la Yordani.

12 Kwa hiyo wana wa Yakobo wakamfanyia kama tu alivyokuwa amewaagiza.+ 13 Wanawe walimbeba na kumpeleka katika nchi ya Kanaani na kumzika katika pango lililo katika shamba la Makpela, shamba lililo mbele ya Mamre ambalo Abrahamu alikuwa amenunua kutoka kwa Efroni Mhiti ili awazike humo watu wake.+ 14 Baada ya kumzika baba yake, Yosefu akarudi Misri pamoja na ndugu zake na wote walioenda naye kumzika baba yake.

15 Ndugu za Yosefu walipoona kwamba baba yao amekufa, wakasema: “Huenda Yosefu ana chuki kutuelekea na atatulipiza uovu wote tuliomtendea.”+ 16 Kwa hiyo wakamtumia Yosefu ujumbe huu: “Baba yako alitoa amri hii kabla ya kifo chake: 17 ‘Hivi ndivyo mtakavyomwambia Yosefu: “Nakusihi, tafadhali, wasamehe ndugu zako uovu wao na dhambi waliyokutendea ili kukudhuru.”’ Sasa, tafadhali, wasamehe watumishi wa Mungu wa baba yako uovu wao.” Na Yosefu akalia walipomwambia hivyo. 18 Kisha ndugu zake wakaja pia na kuanguka mbele yake na kumwambia: “Tazama, sisi ni watumwa wako!”+ 19 Yosefu akawaambia: “Msiogope. Je, nimechukua nafasi ya Mungu? 20 Ingawa mlikusudia kunidhuru,+ Mungu alikusudia hali hiyo ibadilike na kuwa njema na kuokoa maisha ya watu wengi, kama anavyofanya leo.+ 21 Sasa basi msiogope. Nitaendelea kuwapa ninyi na watoto wenu chakula.”+ Kwa hiyo akawafariji na kuwatia moyo.

22 Na Yosefu akaendelea kuishi Misri, yeye na watu wa nyumba ya baba yake; Yosefu aliishi miaka 110. 23 Yosefu akaona kizazi cha tatu cha wana wa Efraimu,+ pia wana wa Makiri,+ mwana wa Manase. Walizaliwa kwenye magoti ya Yosefu.* 24 Mwishowe Yosefu akawaambia ndugu zake: “Ninakufa, lakini kwa hakika Mungu atawakazia uangalifu,+ naye hakika atawapandisha kutoka katika nchi hii na kuwapeleka katika nchi aliyoapa kwamba atawapa Abrahamu, Isaka, na Yakobo.”+ 25 Basi Yosefu akawaapisha wana wa Israeli, akisema: “Kwa hakika Mungu atawakazia ninyi uangalifu. Mnapaswa kuiondoa mifupa yangu huku.”+ 26 Yosefu akafa akiwa na umri wa miaka 110, nao wakampaka dawa ili asioze,+ akawekwa ndani ya jeneza nchini Misri.

Au “ukiwa.”

Au “maji yenye nguvu.”

Au “roho ya Mungu.”

Au “taa.”

Au “nafsi zilizo.”

Au “angani.”

Au “wanyama wakubwa sana.”

Au “nafsi.”

Au “wanyama waendao,” inaonekana wanatia ndani wanyama wanaotambaa na jamii nyingine za wanyama zilizo tofauti na jamii nyinginezo.

Au “ambaye ni nafsi hai.”

Tnn., “na jeshi lake lote likakamilika.”

Hili ndilo andiko la kwanza kutaja jina la pekee la Mungu, יהוה (YHWH). Angalia Nyongeza A4.

Au “nafsi hai.” Kiebrania, neʹphesh, ambalo kihalisi linamaanisha “kiumbe anayepumua.” Angalia Kamusi.

Tnn., “na kuwa vichwa vinne.”

Au “Tigri.”

Au “ataendelea kuwa.”

Au “mjanja; mwenye hila.”

Au “uhasama.”

Tnn., “mbegu yako.”

Tnn., “mbegu yake.”

Au “atakujeruhi; atakugonga.”

Au “utamjeruhi; utamponda.”

Maana yake “Mtu wa Udongo; Binadamu; Mwanadamu.”

Tnn., “mkate.”

Maana yake “Anayeishi.”

Tnn., “na uso wake ukakunjamana.”

Au “hutakwezwa?”

Tnn., “nguvu zake.”

Tnn., “kutoka kwenye uso wa ardhi.”

Au “nchi ya Nodi.”

Au “filimbi.”

Maana yake “Aliyechaguliwa; Aliyesimamishwa.”

Tnn., “mbegu nyingine.”

Au “Adamu; Wanadamu.”

Huenda jina hili linamaanisha “Pumziko; Faraja.”

Msemo wa Kiebrania unaorejelea malaika, wana wa Mungu.

Au labda, “kwa sababu anatenda kulingana na mwili.”

Huenda neno hili linamaanisha “Waangushaji,” yaani, wale wanaowaangusha wengine chini. Angalia Kamusi.

Au “akasikitika.”

Au “naye akaumia moyoni mwake.”

Au “lawama.”

Tnn., “vizazi vyake.”

Tnn., “sanduku”; chombo kikubwa.

Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.

Katika Kiebrania ni tsoʹhar. Baadhi ya watu wanasema kwamba tsoʹhar ni nafasi ya mkono mmoja kati ya paa na dari, si dirisha au nafasi ya kuingizia mwangaza.

Au “roho ya uhai.”

Au labda, “jozi saba za kila mnyama aliye safi.”

Au labda, “jozi saba za viumbe wanaoruka angani.”

Au “roho ya uhai.”

Au “ikaendelea kumwagika.”

Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.

Au “pumzi ya roho ya uhai.”

Tnn., “akamkumbuka.”

Au “ikazuiliwa.”

Au “mahali pa kutua kwa ajili ya wayo wa mguu wake.”

Au “wajae.”

Au “inayotuliza.”

Au “nimewaweka chini ya mamlaka yenu.”

Au “nafsi yake.”

Au “damu ya nafsi zenu.”

Au “nafsi iliyo hai iliyo.”

Au “Viumbe wote walio hai.”

Au “Majiji ya kwanza ya ufalme wake yalikuwa.”

Au labda, “Yanafanyiza lile jiji kubwa.”

Au labda, “ndugu mkubwa wa Yafethi.”

Maana yake “Mgawanyiko.”

Au “wakaaji wa dunia walikuwa wamegawanyika.”

Au “msamiati uleule.”

Maana yake “Vurugu.”

Au “zitajipatia baraka.”

Tnn., “Nitaipa mbegu yako.”

Au “aishi huko akiwa mgeni.”

Au “na nafsi yangu itaendelea kuishi.”

Tnn., “mbegu yako.”

Tnn., “nitaifanya mbegu yako iwe.”

Tnn., “mbegu yako itaweza.”

Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”

Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”

Tnn., “ndugu yake.”

Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”

Tnn., “mbegu yoyote.”

Tnn., “mwana.”

Tnn., “yule anayetoka katika sehemu zako za ndani.”

Tnn., “itakavyokuwa mbegu yako.”

Au “akamhesabia uadilifu.”

Au “na kuweka kila kipande ili kilingane na cha pili.”

Tnn., “mbegu.”

Tnn., “Nitaipa mbegu yako.”

Tnn., “kifuani pako.”

Maana yake “Mungu Husikia.”

Baadhi ya watu hudhani ni pundamilia. Yaelekea ametumiwa kurejelea mtazamo wa kujitegemea.

Au labda, “naye ataishi kwa uhasama na ndugu zake wote.”

Maana yake “Kisima cha Aliye Hai Ambaye Huniona.”

Au “bila lawama.”

Maana yake “Baba Yuko Juu (Amekwezwa).”

Maana yake “Baba wa Umati (Halaiki); Baba wa Wengi.”

Tnn., “mbegu yako.”

Tnn., “mbegu yako.”

Tnn., “mbegu yako.”

Tnn., “mbegu yako.”

Tnn., “mbegu yako.”

Tnn., “mbegu yenu.”

Huenda jina hili linamaanisha “Mgomvi.”

Maana yake “Binti ya Mfalme.”

Maana yake “Kicheko.”

Tnn., “mbegu yake.”

Yaani, malaika aliyemwakilisha Yehova.

Tnn., “mtie nguvu mioyo yenu.”

Tnn., “vipimo vitatu vya sea.” Sea moja ilikuwa sawa na lita 7.33 (vibaba 6.66). Angalia Nyongeza B14.

Yaani, “Alikuwa ameacha kupata hedhi.”

Au “yatajipatia baraka.”

Au “ulinzi wa.”

Au “Wakasongamana kumzunguka Loti.”

Yaani, malaika waliovaa miili ya kibinadamu.

Yaani, malaika waliovaa miili ya kibinadamu.

Au “kimekuwa kikubwa.”

Yaani, malaika waliovaa miili ya kibinadamu.

Yaani, malaika waliomwakilisha Yehova.

Au “upendo mshikamanifu.”

Au “nafsi yangu itaendelea kuishi.”

Maana yake “Udogo.”

Au “kalibu.”

Au “akiishi akiwa mgeni.”

Yaani, hakuwa amefanya naye ngono.

Au “ni adilifu.”

Tnn., “Tazama, ni kifuniko cha macho kwako.”

Au “alikuwa amefunga kabisa kila tumbo la uzazi la nyumba ya Abimeleki.”

Au labda, “atanicheka.”

Tnn., “Isikilize sauti yake.”

Tnn., “ile itakayoitwa mbegu yako itapitia.”

Tnn., “mbegu yako.”

Maana yake “Kisima cha Kile Kiapo; Kisima cha Wale Saba.”

Au “akaishi akiwa mgeni.”

Tnn., “kwa siku nyingi.”

Au “kisu cha kuchinjia.”

Au “kisu cha kuchinjia.”

Maana yake “Yehova Ataandaa; Yehova Atahakikisha Jambo Hilo.”

Tnn., “mbegu.”

Tnn., “mbegu.”

Au “majiji ya.”

Tnn., “mbegu yako.”

Au labda, “kiongozi mkuu.”

Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.

Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.

Tnn., “mbegu yako.”

Tnn., “Akawapigisha magoti ngamia.”

Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.

Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.

Huenda ni Labani.

Tnn., “ili niende mkono wa kulia au wa kushoto.”

Au “Hatuwezi kukuambia jambo jema au baya.”

Yaani, mlezi wake ambaye sasa alikuwa kijakazi wake.

Au “na uwe mama ya maelfu ya makumi ya maelfu.”

Tnn., “mbegu yako imiliki.”

Au “majiji ya.”

Tnn., “akakusanywa kwa watu wake.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.

Au “kambi zao zilizozingirwa na kuta.”

Tnn., “akakusanywa kwa watu wake.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.

Au labda, “Aliishi kwa uhasama na ndugu zake wote.”

Maana yake “Mwenye Nywele Nyingi.”

Maana yake “Anayeshika Kisigino; Anayechukua Nafasi ya Mwingine.”

Tnn., “chekundu, hiki chekundu.”

Au “nina njaa kali.”

Maana yake “Mwekundu.”

Tnn., “mbegu yako.”

Tnn., “mbegu.”

Tnn., “mbegu.”

Tnn., “mbegu.”

Au “akimkumbatia.”

Au “korongo.”

Au “korongoni.”

Maana yake “Ugomvi.”

Maana yake “Shtaka.”

Maana yake “Maeneo Makubwa.”

Tnn., “mbegu.”

Tnn., “uchungu mkali wa rohoni.”

Maana yake “Anayeshika Kisigino; Anayechukua Nafasi ya Mwingine.”

Au “anajifariji kwa mawazo ya kukuua.”

Tnn., “mbegu yako.”

Tnn., “mbegu yako.”

Au “zitajipatia baraka.”

Maana yake “Nyumba ya Mungu.”

Tnn., “ndugu ya.”

Au “mtu wangu wa ukoo niliye na uhusiano wa damu naye.”

Tnn., “ndugu yangu?”

Tnn., “anachukiwa.”

Tnn., “alifungua tumbo lake la uzazi.”

Maana yake “Tazama, Mwana!”

Maana yake “Kusikia.”

Maana yake “Kushikamana; Ungana.”

Maana yake “Aliyesifiwa; Kitu cha Kusifiwa.”

Au “amekunyima uzao wa tumbo lako la uzazi?”

Tnn., “azae kwenye magoti yangu.”

Maana yake “Mwamuzi.”

Maana yake “Mieleka Yangu.”

Maana yake “Neema.”

Maana yake “Mwenye Furaha; Furaha.”

Au “mshahara wa mtu aliyekodiwa.”

Maana yake “Yeye Ni Mshahara.”

Maana yake “Kuvumilia.”

Tnn., “na Mungu akamsikiliza na kufungua tumbo lake la uzazi.”

Ufupisho wa jina Yosifia, linalomaanisha “Yah na Aongeze.”

Au “mambo niliyoshuhudia yamenisaidia.”

Au “unyoofu.”

Au “miungu ya familia; sanamu.”

Yaani, Mto Efrati.

Au “watu wake wa ukoo.”

Tnn., “wana.”

Tnn., “desturi ya wanawake imenijia.”

Tnn., “woga wa Isaka.”

Neno la Kiaramu linalomaanisha “Rundo la Ushahidi.”

Neno la Kiebrania linalomaanisha “Rundo la Ushahidi.”

Tnn., “kwa woga wa Isaka baba yake.”

Tnn., “mkate.”

Maana yake “Kambi Mbili.”

Tnn., “shamba.”

Au “Nimeishi kama mgeni.”

Tnn., “mbegu.”

Au “bonde la mto; korongo.”

Maana yake “Anayepambana na (Anayestahimili Pamoja na) Mungu” au “Mungu Hupambana.”

Maana yake “Uso wa Mungu.”

Au “nafsi yangu imehifadhiwa.”

Au “Penieli.”

Tnn., “kano ya mshipa wa paja.”

Maana yake “Mabanda; Vibanda.”

Au “kuwaona.”

Tnn., “kuzungumza na moyo wa msichana huyo.”

Au “nafsi ya mwanangu Shekemu imeshikamana na.”

Au “na muoane nasi.”

Tnn., “aliye na govi.”

Au “Mmenifanya nitengwe.”

Au “katika njia niliyotembea.”

Au “akavificha.”

Maana yake “Mungu wa Betheli.”

Maana yake “Mwaloni wa Kilio.”

Tnn., “watatoka katika kiuno chako.”

Tnn., “mbegu yako.”

Maana yake “Mwana wa Maombolezo Yangu.”

Maana yake “Mwana wa Mkono wa Kulia.”

Tnn., “Akakusanywa kwa watu wake.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.

Tnn., “akiwa amezeeka na akiwa amejaa siku.”

Au “walimoishi wakiwa wageni.”

Shehe alikuwa mkuu wa kabila.

Tnn., “wana wa Israeli.”

Tnn., “shamba.”

Au “nguo ndefu maridadi.”

Au “nchi tambarare ya chini ya.”

Au “msimguse.”

Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.

Maana yake “Mpasuko,” labda linarejelea hali ya kupasuka msamba.

Yaani, bwana wa Yosefu.

Tnn., “siku kadhaa.”

Au “fasiri yake.”

Au “hatuna mfasiri.”

Tnn., “atakiinua juu kichwa chako.”

Tnn., “ndani ya tangi la maji; shimoni.”

Au “amefasiri.”

Au “amefasiri.”

Au “fasiri yake.”

Au “alivyotufasiria.”

Tnn., “ndani ya tangi la maji; shimoni.”

Au “inapohusu tu kiti cha ufalme.”

Inaonekana ni neno linalowaamuru watu waonyeshe heshima na staha.

Tnn., “kuinua mkono wake au mguu wake.”

Yaani, Heliopolisi.

Au “kutembea kotekote katika.”

Tnn., “aliposimama mbele ya.”

Au “Heliopolisi.”

Maana yake “Anayesahaulisha; Anayemfanya Mwingine Asahau.”

Maana yake “Anayezaa Maradufu.”

Au “mkate.”

Au “mkate.”

Tnn., “Msitende dhambi dhidi ya mtoto huyu.”

Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.

Au “rehani kwa ajili yake.”

Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.

Au “nafsi yake imefungamana na nafsi ya.”

Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.

Au “nchini.”

Tnn., “kuwa kama baba.”

Tnn., “akamwangukia shingoni.”

Au “mtaishi kwa kutegemea.”

Au “sehemu nono ya.”

Au “watu wake wote.”

Yaani, atayafumba Yakobo atakapokufa.

Au “wana wa Israeli.”

Yaani, Heliopolisi.

Tnn., “Wana.” Huenda alikuwa na wana wengine ambao majina yao hayatajwi.

Tnn., “akamwangukia shingoni.”

Au “na kumlilia shingoni tena na tena.”

Au “nikihamahama; nikikaa kama mgeni.”

Au “wakihamahama; wakikaa kama wageni.”

Tnn., “mkate.”

Tnn., “mkate.”

Tnn., “Nitakapolala na baba zangu.”

Tnn., “nitaipa mbegu yako.”

Tnn., “mbegu yako.”

Tnn., “mbegu yake italingana.”

Au “mteremko mmoja zaidi wa nchi.” Tnn., “bega moja zaidi.”

Au “ulikitia unajisi.”

Angalia Kamusi.

Au labda, “mtazamo wangu.”

Maana yake “Yule Ambaye Ni Yake; Yule Ambaye Ni Mali Yake.”

Au “Chakula cha Asheri kitakuwa kingi sana.”

Yaani, Yosefu.

Tnn., “Nakusanywa kwa watu wangu.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.

Tnn., “akakusanywa kwa watu wake.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.

Au “nyumba.”

Maana yake “Maombolezo ya Wamisri.”

Yaani, aliwatendea kama wanawe na kwa njia ya pekee.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki