Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • bi12 Yoshua 1:1-24:33
  • Yoshua

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yoshua
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Yoshua

Yoshua

1 Basi ikawa kwamba baada ya kifo cha Musa mtumishi wa Yehova, Yehova akamwambia Yoshua+ mwana wa Nuni, mhudumu+ wa Musa: 2 “Musa mtumishi wangu amekufa;+ basi simama sasa, vuka huu mto Yordani, wewe na watu hawa wote, mwingie katika nchi ambayo ninawapa wao, wana wa Israeli.+ 3 Kila mahali ambapo wayo wa mguu wenu utakanyaga, nitawapa ninyi mahali hapo, kama vile nilivyomwahidi Musa.+ 4 Na eneo lenu litakuwa kutoka nyika hii na huu mlima Lebanoni mpaka ule mto mkubwa, mto Efrati, yaani, nchi yote ya Wahiti,+ na mpaka kwenye ile Bahari Kuu upande wa magharibi.+ 5 Hakuna yeyote atakayesimama imara mbele yako siku zote za maisha yako.+ Nitakuwa pamoja nawe,+ kama vile nilivyokuwa pamoja na Musa. Sitakutupa wala kukuacha kabisa.+ 6 Uwe hodari na mwenye nguvu,+ kwa maana ni wewe utakayewafanya watu hawa wairithi+ ile nchi ambayo niliwaapia mababu zao kuwa nitawapa.+

7 “Ila tu uwe hodari na mwenye nguvu sana ili uangalie kufanya kulingana na sheria yote ambayo Musa mtumishi wangu alikuamuru.+ Usiiache, kwenda upande wa kuume wala wa kushoto,+ kusudi utende kwa hekima kila mahali unapoenda.+ 8 Kitabu hiki cha sheria kisiondoke katika kinywa chako,+ nawe ukisome kwa sauti ya chini mchana na usiku, upate kuangalia kufanya kulingana na yote ambayo yameandikwa ndani yake;+ kwa maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha utatenda kwa hekima.+ 9 Je, mimi sikukuamuru wewe?+ Uwe hodari na mwenye nguvu. Usitetemeke wala usiwe na hofu,+ kwa maana Yehova Mungu wako yupo pamoja nawe kila mahali unapoenda.”+

10 Ndipo Yoshua akawaamuru maofisa wa watu, akisema: 11 “Piteni katikati ya kambi na kuwaamuru watu, mkisema, ‘Jitayarishieni chakula, kwa kuwa siku tatu kutoka sasa mtavuka huu mto Yordani ili kuingia na kuimiliki nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa ninyi mpate kuimiliki.’”+

12 Kisha Yoshua akawaambia Warubeni na Wagadi na nusu ya kabila la Manase: 13 “Kumbukeni neno lile ambalo Musa mtumishi wa Yehova aliwaamuru,+ akisema, ‘Yehova Mungu wenu anawapa ninyi pumziko naye amewapa nchi hii. 14 Wake zenu, watoto wenu wadogo na mifugo yenu, watakaa katika nchi ambayo Musa amewapa ninyi ng’ambo hii ya Yordani;+ lakini ninyi wanaume mtavuka mkiwa mmejipanga kivita+ mbele ya ndugu zenu, wanaume wote ambao ni mashujaa wenye nguvu,+ nanyi mtawasaidia. 15 Kwanza Yehova atakapowapa ndugu zenu pumziko kama vile alivyowapa ninyi, nao pia wawe wameirithi nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa,+ ndipo mtakaporudi katika nchi ya urithi wenu na kuimiliki,+ nchi ile ambayo Musa mtumishi wa Yehova amewapa ng’ambo ya Yordani upande wa mashariki.’”+

16 Basi wakamjibu Yoshua, wakisema: “Yote ambayo umetuamuru tutafanya, na popote utakapotutuma tutaenda.+ 17 Kama vile tulivyomsikiliza Musa katika kila jambo, ndivyo tutakavyokusikiliza wewe. Ila tu Yehova Mungu wako na awe pamoja nawe+ kama vile alivyokuwa pamoja na Musa.+ 18 Mtu yeyote atakayeasi agizo lako,+ akatae kuyasikiliza maneno yako katika mambo yote ambayo utamwamuru, atauawa.+ Ila tu uwe hodari na mwenye nguvu.”+

2 Kisha Yoshua mwana wa Nuni akatuma kisiri wanaume wawili kutoka Shitimu,+ waende wakiwa wapelelezi, akawaambia: “Nendeni, angalieni nchi na Yeriko.” Basi wakaenda wakafika nyumbani kwa mwanamke mmoja kahaba ambaye jina lake lilikuwa Rahabu,+ nao wakakaa humo. 2 Baada ya muda mfalme wa Yeriko akaambiwa hivi: “Tazama! Wanaume kutoka kwa wana wa Israeli wameingia humu leo usiku ili kuipeleleza nchi.” 3 Ndipo mfalme wa Yeriko akatuma watu kwa Rahabu, akisema: “Watoe nje wale wanaume waliokuja kwako, walioingia katika nyumba yako, kwa maana wamekuja kwa kusudi la kuipeleleza nchi nzima.”+

4 Wakati huohuo mwanamke huyo akawachukua wale wanaume wawili, akawaficha. Kisha akasema: “Ni kweli, wanaume hao walikuja kwangu, lakini sikujua walikotoka. 5 Ikawa wakati wa kufungwa kwa lango,+ kulipokuwa na giza, wanaume wale wakatoka. Wala sijui walikokwenda. Wafuatilieni haraka, kwa maana mtawafikia.” 6 (Lakini alikuwa amewapandisha darini,+ naye akawaficha kati ya majani ya kitani yaliyokuwa yametandikwa kwa mistari kwa ajili yake juu ya dari.) 7 Basi watu hao wakawafuatilia kuelekea upande wa Yordani vivukoni,+ nao wakalifunga lango mara moja baada ya wale waliowafuatilia kuondoka.

8 Kabla hawajalala akaenda kwao juu ya dari. 9 Naye akawaambia wanaume hao: “Najua hakika ya kwamba Yehova atawapa nchi hii,+ na ya kwamba tumeshikwa na hofu kwa sababu yenu,+ na ya kwamba wakaaji wote wa nchi wamevunjika moyo kwa sababu yenu.+ 10 Kwa maana tumesikia jinsi ambavyo Yehova aliyakausha maji ya Bahari Nyekundu mbele yenu wakati mlipotoka Misri,+ na yale mliyowatendea wale wafalme wawili wa Waamori waliokuwa ng’ambo ile nyingine ya Yordani, yaani, Sihoni+ na Ogu,+ ambao mliwaangamiza.+ 11 Tuliposikia hayo, ndipo mioyo yetu ikaanza kuyeyuka,+ wala roho yoyote haijaamka bado ndani ya mtu yeyote kwa sababu yenu,+ kwa kuwa Yehova Mungu wenu ni Mungu juu mbinguni na chini duniani.+ 12 Basi sasa, tafadhali, niapieni kwa Yehova+ kwamba, kwa kuwa nimewatendea ninyi fadhili zenye upendo, ninyi pia kwa hakika mtaitendea nyumba ya baba yangu+ kwa fadhili zenye upendo, tena mnipe ishara+ yenye kuaminika. 13 Nanyi mtawahifadhi hai baba yangu+ na mama yangu na ndugu zangu na dada zangu na watu wao wote, nanyi mtazikomboa nafsi zetu kutoka katika kifo.”+

14 Ndipo wanaume hao wakamwambia: “Nafsi zetu na zife badala yenu!+ Ikiwa hamtasema juu ya hii shughuli yetu, itatukia kwamba wakati Yehova atakapotupa nchi hii, sisi pia tutakutendea kwa fadhili zenye upendo na kwa uaminifu.”+ 15 Baada ya hayo akawashusha kwa kamba kupitia dirishani, kwa kuwa nyumba yake ilikuwa upande wa ukuta, naye alikuwa akikaa ukutani.+ 16 Naye akawaambia: “Nendeni katika eneo lenye milima, ili wale wanaowafuatilia wasije wakawapata; nanyi mjifiche huko siku tatu, mpaka wale wanaowafuatilia wawe wamerudi, kisha mwende zenu baadaye.”

17 Nao wale wanaume wakamwambia: “Hatuna hatia kuhusiana na kiapo chako hiki ambacho umetuapisha.+ 18 Tazama! Tutaingia katika nchi hii. Funga kamba hii ya uzi mwekundu katika dirisha ambalo ulitushushia, na baba yako na mama yako na ndugu zako na nyumba yote ya baba yako uwakusanye kwako ndani ya nyumba.+ 19 Na itatukia kwamba mtu yeyote atakayeondoka katika milango ya nyumba yako na kwenda nje,+ damu yake itakuwa juu ya kichwa chake mwenyewe, nasi hatutakuwa na hatia; na kila mtu atakayeendelea kukaa nawe ndani ya nyumba, damu yake itakuwa juu ya vichwa vyetu ikiwa mkono utanyooshwa juu yake. 20 Nawe ukitoa habari ya hii shughuli yetu,+ sisi pia hatutakuwa na hatia kuhusiana na hiki kiapo chako ulichotuapisha.” 21 Naye akasema: “Na iwe hivyo kulingana na maneno yenu.”

Kwa hiyo akawaacha waende, nao wakaenda zao. Kisha akafunga ile kamba nyekundu dirishani. 22 Basi wakaenda na kufika katika eneo lenye milima, wakakaa huko siku tatu, mpaka wale wenye kuwafuatilia walipokuwa wamerudi. Basi wale wenye kuwafuatilia walikuwa wakiwatafuta katika kila barabara, lakini hawakuwaona. 23 Kisha wale wanaume wawili wakashuka tena kutoka katika eneo lenye milima, wakavuka na kwenda kwa Yoshua mwana wa Nuni, nao wakaanza kumweleza mambo yote yaliyowapata. 24 Nao wakamwambia Yoshua: “Yehova ameitia nchi yote mkononi mwetu.+ Na kwa hiyo wakaaji wote wa nchi wamevunjika moyo pia kwa sababu yetu.”+

3 Ndipo Yoshua akaamka asubuhi na mapema, yeye pamoja na wana wote wa Israeli wakaanza safari kutoka Shitimu,+ wakafika Yordani; nao wakalala hapo usiku kucha kabla ya kuvuka.

2 Basi ikawa mwishoni mwa siku tatu,+ maofisa+ wakapita katikati ya kambi 3 wakawaamuru watu, wakisema: “Mara mtakapoliona sanduku la agano la Yehova Mungu wenu, na makuhani Walawi wakiwa wamelichukua,+ ndipo mtakapoondoka mahali penu, nanyi mlifuate, 4 —ila mwache kuwe na umbali wa karibu kipimo cha mikono elfu mbili kati yenu na sanduku hilo;+ msilikaribie—ili mpate kuijua njia mnayopaswa kutembea, kwa maana hamjapata kuipita njia hiyo hapo mbeleni.”

5 Sasa Yoshua akawaambia watu: “Jitakaseni,+ kwa maana kesho Yehova atafanya mambo ya ajabu katikati yenu.”+

6 Kisha Yoshua akawaambia makuhani: “Chukueni sanduku la agano,+ na mpite mbele ya watu.” Basi wakachukua sanduku la agano, wakapita mbele ya watu.

7 Ndipo Yehova akamwambia Yoshua: “Leo nitaanza kukufanya uwe mkuu machoni pa Israeli wote,+ ili wajue kwamba nitakuwa pamoja nawe+ kama vile nilivyokuwa pamoja na Musa.+ 8 Na wewe—waamuru+ makuhani wanaolichukua sanduku la agano, ukisema, ‘Mara mtakapofika kwenye ukingo wa maji ya Yordani, simameni+ katika Yordani.’”

9 Ndipo Yoshua akaendelea kuwaambia wana wa Israeli: “Karibieni hapa, msikilize maneno ya Yehova Mungu wenu.” 10 Kisha Yoshua akasema: “Kwa jambo hili mtajua kwamba Mungu aliye hai yupo katikati yenu,+ na kwamba bila shaka atawafukuzia mbali kutoka mbele yenu Wakanaani na Wahiti na Wahivi na Waperizi na Wagirgashi na Waamori na Wayebusi.+ 11 Tazameni! sanduku la agano la Bwana wa dunia yote linapita mbele yenu kuingia Yordani. 12 Basi sasa jichukulieni wanaume kumi na wawili kutoka katika makabila ya Israeli, kila kabila mwanamume mmoja.+ 13 Na itatukia kwamba mara tu nyayo za miguu ya makuhani wanaolichukua sanduku la Yehova, Bwana wa dunia yote, zitakapokanyaga maji ya Yordani, maji ya Yordani yatazuiliwa, maji yanayoshuka kutoka juu, nayo yatasimama kama ukuta wa maji.”+

14 Basi ikawa watu walipotoka katika mahema yao kabla tu ya kuvuka Yordani, nao makuhani wakiwa wamelichukua sanduku+ la agano mbele ya watu, 15 mara tu wachukuaji wa lile Sanduku walipofika Yordani na miguu ya makuhani waliolichukua Sanduku ilipotumbukizwa katika maji ya ukingoni (maana Yordani hufurika kingo+ zake zote siku zote za mavuno), 16 ndipo maji yanayoshuka kutoka juu yakaanza kusimama. Yakasimama kama ukuta wa maji+ mbali sana huko Adamu, jiji lililo kando ya Sarethani,+ na yale yanayoshuka kuelekea bahari ya Araba, yaani, Bahari ya Chumvi,+ yakaisha. Yalizuiliwa kabisa, na watu wakavuka mbele ya Yeriko. 17 Wakati huohuo wale makuhani waliolichukua sanduku la agano la Yehova wakaendelea kusimama bila kusonga kwenye nchi kavu+ katikati ya Yordani, huku Israeli wote wakivuka juu ya nchi kavu,+ mpaka taifa zima lilipokuwa limemaliza kuvuka Yordani.

4 Kisha ikawa kwamba mara tu taifa zima lilipokuwa limemaliza kuvuka Yordani,+ Yehova akamwambia Yoshua: 2 “Jichukulieni wanaume kumi na wawili kutoka kati ya watu, kila kabila mwanamume mmoja,+ 3 na kuwaamuru, mkisema, ‘Jichukulieni mawe kumi na mawili+ kutoka katikati ya Yordani, kutoka mahali ambapo miguu ya makuhani ilisimama,+ nanyi myachukue na kuyaweka katika makao+ mtakayokaa usiku huu.’”

4 Basi Yoshua akawaita wanaume kumi na wawili+ ambao alikuwa amechagua kutoka kati ya wana wa Israeli, kila kabila mwanamume mmoja; 5 kisha Yoshua akawaambia: “Piteni mbele ya sanduku la Yehova Mungu wenu mpaka katikati ya Yordani, na mjichukulie kila mmoja wenu jiwe moja begani mwake, kulingana na hesabu ya makabila ya wana wa Israeli, 6 ili kwamba jambo hili liwe ishara katikati yenu.+ Ikiwa wana wenu watauliza wakati ujao, wakisema, ‘Kwa nini mna mawe haya?’+ 7 Ndipo mtakapowaambia, ‘Kwa sababu maji ya Yordani yalizuiliwa kabisa kutoka mbele ya sanduku la agano la Yehova.+ Lilipopita kati ya Yordani, maji ya Yordani yalizuiliwa kabisa, na mawe haya yatakuwa ukumbusho kwa wana wa Israeli mpaka wakati usio na kipimo.’”+

8 Basi wana wa Israeli wakafanya hivyo, kama vile Yoshua alivyokuwa ameamuru, nao wakachukua mawe kumi na mawili kutoka katikati ya Yordani, kama vile Yehova alivyokuwa amemwambia Yoshua, ili yalingane na hesabu ya makabila ya wana wa Israeli;+ nao wakayachukua na kuyapeleka kwenye yale makao+ na kuyaweka huko.

9 Pia kulikuwa na mawe kumi na mawili ambayo Yoshua alipanga katikati ya Yordani katika mahali pale iliposimama+ miguu ya wale makuhani waliochukua sanduku la agano, nayo yangali hapo mpaka leo hii.

10 Na wale makuhani waliolichukua Sanduku walikuwa wamesimama katikati+ ya Yordani mpaka shughuli hiyo yote ambayo Yehova alikuwa amemwamuru Yoshua awaambie watu ilipomalizika, kulingana na yote ambayo Musa alikuwa amemwamuru Yoshua.+ Na wakati huo wote watu wakafanya haraka+ na kuvuka. 11 Kisha ikawa kwamba mara tu watu wote walipokuwa wamemaliza kuvuka, sanduku+ la Yehova likavuka, na hao makuhani, mbele ya watu. 12 Kisha wana wa Rubeni na wana wa Gadi na nusu ya kabila la Manase+ wakavuka wakiwa wamejipanga kivita+ machoni pa wana wa Israeli, kama vile Musa alivyokuwa amewaambia.+ 13 Karibu watu 40,000 waliotayarishwa kijeshi wakavuka mbele za Yehova kwa ajili ya vita kwenda katika nchi tambarare za jangwa la Yeriko.

14 Siku hiyo Yehova alimfanya Yoshua kuwa mkuu machoni pa Israeli wote,+ nao wakaanza kumwogopa kama vile walivyokuwa wakimwogopa Musa siku zote za maisha yake.+

15 Ndipo Yehova akamwambia Yoshua: 16 “Waamuru makuhani wanaochukua sanduku la ushuhuda+ kwamba wapande kutoka ndani ya Yordani.” 17 Basi Yoshua akawaamuru makuhani, akisema: “Pandeni kutoka ndani ya Yordani.” 18 Kisha ikawa kwamba makuhani waliolichukua sanduku+ la agano la Yehova walipopanda kutoka katikati ya Yordani nao makuhani wakainua miguu+ yao na kukanyaga kwenye nchi kavu, ndipo maji ya Yordani yakaanza kurudi mahali pake na kufanya kingo zake zote zifurike+ kama hapo mwanzoni.

19 Na watu hao wakapanda kutoka katika Yordani siku ya kumi ya mwezi wa kwanza, wakapiga kambi kule Gilgali+ kwenye mpaka wa mashariki wa Yeriko.

20 Kisha Yoshua akapanga katika Gilgali yale mawe kumi na mawili, ambayo walikuwa wamechukua kutoka katika Yordani.+ 21 Naye akawaambia wana wa Israeli: “Wana wenu watakapowauliza baba zao wakati ujao, wakisema, ‘Mawe haya yanamaanisha nini?’+ 22 Ndipo mtakapowajulisha wana wenu, mkisema, ‘Israeli walivuka huu mto Yordani ukiwa nchi kavu,+ 23 Yehova Mungu wenu alipoyakausha maji ya Yordani mbele yao mpaka walipokwisha kuvuka, kama vile Yehova Mungu wenu alivyokuwa ameifanya Bahari Nyekundu alipoikausha mbele yetu mpaka tulipokwisha kuvuka;+ 24 ili watu wote wa dunia wapate kuujua mkono wa Yehova,+ kwamba ni wenye nguvu;+ ili mpate kumwogopa Yehova Mungu wenu sikuzote.’”+

5 Na ikawa kwamba, mara tu wafalme wote wa Waamori,+ waliokuwa ng’ambo ya Yordani upande wa magharibi, na wafalme wote wa Wakanaani,+ waliokuwa kando ya bahari, waliposikia kwamba Yehova alikuwa amekausha maji ya Yordani mbele ya wana wa Israeli mpaka walipokuwa wamevuka, ndipo mioyo yao ikaanza kuyeyuka,+ wala haikuwamo roho yoyote ya nguvu iliyobaki ndani yao tena kwa sababu ya wana wa Israeli.+

2 Na wakati huo Yehova akamwambia Yoshua: “Jitengenezee visu vya jiwe gumu, uwatahiri+ tena wana wa Israeli mara ya pili.” 3 Basi Yoshua akajitengenezea visu vya jiwe gumu, akawatahiri wana wa Israeli katika Gibeath-haaralothi.+ 4 Na hii ndiyo sababu iliyomfanya Yoshua awatahiri: watu wote waliotoka Misri, waume, wanaume wote wa vita, walikuwa wamekufa+ njiani katika nyika walipokuwa wakitoka Misri. 5 Kwa maana watu wote waliotoka walikuwa wametahiriwa, lakini watu wote waliozaliwa katika nyika njiani walipokuwa wakitoka Misri hawakuwa wamewatahiri. 6 Kwa maana wana wa Israeli walikuwa wametembea miaka 40+ nyikani, mpaka lilipokwisha taifa lote la wale wanaume wa vita waliotoka Misri ambao hawakuisikiliza sauti ya Yehova, ambao Yehova alikuwa amewaapia kwamba hatawaruhusu kamwe waione nchi+ ambayo Yehova alikuwa amewaapia mababu zao kwamba atatupa sisi,+ nchi inayotiririka maziwa na asali.+ 7 Naye akawasimamisha wana wao badala yao.+ Yoshua akawatahiri hao wana, kwa sababu walikuwa hawajatahiriwa, kwa maana hawakuwa wamewatahiri njiani.

8 Kisha ikawa kwamba walipokuwa wamemaliza kutahiri taifa lote, wakaendelea kukaa mahali pao kambini mpaka walipopona.+

9 Ndipo Yehova akamwambia Yoshua: “Leo nimeondolea mbali aibu ya Misri itoke juu yenu.”+ Basi jina la mahali hapo likaitwa Gilgali+ mpaka leo hii.

10 Na wana wa Israeli wakaendelea kupiga kambi katika Gilgali, nao wakasherehekea pasaka siku ya kumi na nne ya mwezi huo,+ wakati wa jioni, katika nchi tambarare za jangwa la Yeriko. 11 Nao wakaanza kula mazao ya nchi siku iliyofuata pasaka, keki zisizo na chachu+ na nafaka zilizochomwa, siku ileile. 12 Ndipo mana ikaacha kuanguka siku iliyofuata walipokuwa wamekula mazao ya nchi, wala mana haikuja tena kwa ajili ya wana wa Israeli,+ nao wakaanza kula mazao ya nchi ya Kanaani mwaka huo.+

13 Kisha ikawa kwamba Yoshua alipokuwa karibu na Yeriko, akainua macho yake na kuangalia, na tazama, palikuwa na mwanamume+ aliyesimama mbele yake akiwa na upanga uliochomolewa mkononi mwake.+ Kwa hiyo Yoshua akamwendea na kumwambia: “Je, wewe uko upande wetu au upande wa adui zetu?” 14 Ndipo yeye akasema: “Hapana, lakini mimi—nikiwa mkuu wa jeshi la Yehova nimekuja sasa.”+ Basi Yoshua akaanguka kifudifudi,+ akasujudu na kumwambia: “Bwana wangu anamwambia nini mtumishi wake?” 15 Ndipo mkuu wa jeshi la Yehova akamwambia Yoshua: “Vua viatu vyako kutoka miguuni mwako, kwa sababu mahali ambapo umesimama ni patakatifu.” Yoshua akavua mara moja.+

6 Basi jiji la Yeriko lilikuwa limefungwa imara kwa sababu ya wana wa Israeli, hakuna mtu aliyetoka nje wala kuingia ndani.+

2 Na Yehova akamwambia Yoshua: “Tazama, nimetia mkononi mwako Yeriko na mfalme wake, na mashujaa, wanaume wenye nguvu.+ 3 Nanyi nyote wanaume wa vita mtapiga mwendo kulizunguka jiji, mkilizunguka jiji mara moja. Hivyo ndivyo utakavyofanya kwa siku sita. 4 Na makuhani saba wachukue pembe saba za kondoo-dume, mbele ya hilo Sanduku, na siku ya saba mpige mwendo kuzunguka jiji mara saba, nao makuhani wazipige pembe.+ 5 Na itatukia kwamba watakapopiga pembe ya kondoo-dume, mtakapoisikia sauti ya pembe, watu wote watapaaza kelele kubwa za vita;+ na ukuta wa jiji utaanguka chini,+ kisha watu watapanda, kila mmoja akisonga mbele moja kwa moja.”

6 Basi Yoshua mwana wa Nuni akawaita makuhani+ na kuwaambia: “Lichukueni sanduku la agano,+ na makuhani saba wachukue pembe saba za kondoo-dume mbele ya sanduku+ la Yehova.” 7 Naye akaendelea kuwaambia watu: “Piteni, mpige mwendo kulizunguka jiji, na kikosi kilichotayarishwa kwa ajili ya vita+ kipite mbele ya sanduku la Yehova.” 8 Basi ikawa kama vile Yoshua alivyowaambia watu; na makuhani saba waliochukua pembe saba za kondoo-dume mbele za Yehova wakapita na kuzipiga pembe hizo, nalo sanduku la agano la Yehova lilikuwa likiwafuata. 9 Na kile kikosi kilichotayarishwa kwa ajili ya vita kilikuwa kinaenda mbele ya makuhani waliokuwa wakizipiga pembe, na wakati huohuo kikosi cha nyuma+ kilikuwa kikilifuata Sanduku nazo zile pembe zilikuwa zikipigwa kwa mfululizo.

10 Basi Yoshua alikuwa amewaamuru watu,+ akisema: “Msipaaze sauti wala kuacha sauti zenu zisikike, na neno lolote lisitoke katika vinywa vyenu mpaka siku nitakapowaambia, ‘Paazeni sauti!’ Ndipo mtakapopaaza sauti.”+ 11 Naye akalipeleka sanduku la agano la Yehova lizunguke jiji, likazunguka mara moja, kisha wakaenda kambini na kukaa usiku kucha katika kambi.

12 Ndipo Yoshua akaamka asubuhi na mapema,+ nao makuhani wakalichukua sanduku+ la Yehova, 13 na makuhani saba waliochukua pembe saba za kondoo-dume mbele ya sanduku la Yehova walikuwa wanatembea, wakizipiga pembe kwa mfululizo, na kile kikosi kilichotayarishwa kwa ajili ya vita kilikuwa kinatembea mbele yao, huku kile kikosi cha nyuma kikifuata sanduku la Yehova nazo pembe zilikuwa zikipigwa kwa mfululizo.+ 14 Nao wakalizunguka jiji siku ya pili mara moja, kisha wakarudi kambini. Hivyo ndivyo walivyofanya kwa siku sita.+

15 Kisha, katika siku ya saba wakaamka mapema, mara kulipopambazuka, nao wakalizunguka jiji vivyo hivyo mara saba. Siku hiyo peke yake walizunguka jiji mara saba.+ 16 Na ikawa kwamba mara ya saba makuhani walipiga pembe, ndipo Yoshua akawaambia watu: “Paazeni sauti;+ kwa maana Yehova amewapa ninyi jiji hili.+ 17 Na jiji hili litakuwa kitu cha kuharibiwa;+ jiji lenyewe pamoja na kila kitu kilicho ndani yake ni vya Yehova. Rahabu+ yule kahaba peke yake ndiye atakayeendelea kuishi, yeye na wote walio pamoja naye katika nyumba, kwa kuwa aliwaficha wajumbe tuliowatuma.+ 18 Nanyi mjiepushe tu na kitu kilichotengwa kwa ajili ya kuharibiwa,+ msije mkawa na tamaa+ na kuchukua sehemu ya vitu vilivyotengwa kwa ajili ya kuharibiwa+ na kuifanya kambi ya Israeli kuwa kitu kilichotengwa kwa ajili ya kuharibiwa na kuiletea laana.+ 19 Lakini fedha yote na dhahabu na vyombo vya shaba na chuma ni vitu vitakatifu kwa Yehova.+ Viwekwe katika hazina ya Yehova.”+

20 Ndipo watu wakapaaza sauti, walipopiga pembe.+ Kisha ikawa kwamba mara tu watu walipoisikia sauti ya pembe na watu wakapaaza kelele kubwa za vita, ndipo ukuta ukaanza kuanguka chini kabisa.+ Kisha watu wakapanda juu, wakaingia katika jiji, kila mmoja akasonga mbele moja kwa moja, na kuliteka jiji. 21 Wakaangamiza kila kitu kilichokuwa ndani ya jiji hilo, kuanzia mwanamume mpaka mwanamke, kuanzia kijana mpaka mzee hata ng’ombe na kondoo na punda, kwa makali ya upanga.+

22 Na Yoshua akawaambia wale wanaume wawili waliokuwa wameipeleleza nchi: “Ingieni katika nyumba ya yule mwanamke, yule kahaba, mkamtoe nje mwanamke huyo na wote walio wake, kama vile mlivyomwapia.”+ 23 Basi wale vijana waliokuwa wamefanya upelelezi wakaingia, wakamtoa nje Rahabu na baba yake na mama yake na ndugu zake na wote waliokuwa wake, ndiyo, wakawatoa nje jamaa zake wote;+ nao wakawaweka nje ya kambi ya Israeli.

24 Kisha wakaliteketeza jiji kwa moto na kila kitu kilichokuwamo.+ Isipokuwa fedha na dhahabu na vyombo vya shaba na chuma wakaviweka katika hazina ya nyumba ya Yehova.+ 25 Naye Yoshua akawahifadhi hai Rahabu yule kahaba na nyumba ya baba yake na wote waliokuwa wake;+ naye anakaa katikati ya Israeli mpaka leo hii,+ kwa sababu aliwaficha wajumbe ambao Yoshua aliwatuma kupeleleza Yeriko.+

26 Ndipo Yoshua akatangaza kiapo wakati huo, akasema: “Na alaaniwe mbele za Yehova mtu yule atakayesimama na kujenga jiji hili, yaani, Yeriko. Kwa kufiwa na mzaliwa wake wa kwanza na auweke msingi wake, na kwa kufiwa na mwana wake aliye mdogo zaidi na aisimamishe milango yake.”+

27 Basi Yehova akawa pamoja na Yoshua,+ na sifa yake ikaenea katika dunia yote.+

7 Kisha wana wa Israeli wakafanya tendo la kukosa uaminifu kuhusiana na kitu kilichotengwa kwa ajili ya kuharibiwa kwa kuwa Akani+ mwana wa Karmi, mwana wa Zabdi, mwana wa Zera, wa kabila la Yuda, alichukua sehemu ya vitu vilivyotengwa kwa ajili ya kuharibiwa.+ Ndipo hasira ya Yehova ikawaka juu ya wana wa Israeli.+

2 Basi Yoshua akatuma wanaume kutoka Yeriko kwenda Ai,+ jiji lililo karibu na Beth-aveni,+ upande wa mashariki wa Betheli,+ na kuwaambia: “Pandeni juu, mkaipeleleze nchi.” Basi wanaume hao wakapanda, wakapeleleza Ai.+ 3 Kisha wakarudi kwa Yoshua wakamwambia: “Usiache watu wote waende. Acha wanaume elfu mbili hivi au wanaume elfu tatu hivi waende kupiga Ai. Usiwachoshe watu wote kwa kuwapeleka huko, kwa maana watu hao ni wachache.”

4 Basi karibu wanaume elfu tatu kati ya watu wakaenda huko, lakini wakakimbia mbele ya wanaume wa Ai.+ 5 Na wanaume wa Ai wakawapiga na kuwaua karibu watu 36 kati yao, wakawafuatilia+ kutoka mbele ya lango mpaka Shebarimu, wakaendelea kuwapiga na kuwaua kwenye mteremko. Basi mioyo ya watu ikaanza kuyeyuka, ikawa kama maji.+

6 Ndipo Yoshua akararua nguo zake za kujitanda, akaanguka kifudifudi+ mbele ya sanduku la Yehova mpaka jioni, yeye na wanaume wazee wa Israeli, nao wakawa wakitia mavumbi vichwani mwao.+ 7 Kisha Yoshua akasema: “Ole wangu, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, kwa nini uliwaleta watu hawa njia yote hiyo kuuvuka Yordani, ili tu kututia mkononi mwa Waamori, watuangamize? Laiti tungejichagulia wenyewe tuendelee kukaa ng’ambo ile nyingine ya Yordani!+ 8 Nakuomba radhi, Ee Yehova, lakini niseme nini baada ya Israeli kugeuza mgongo wake mbele ya adui zake? 9 Nao Wakanaani na wakaaji wote wa nchi hii watasikia habari hizi, nao hakika watatuzunguka na kulikatilia mbali jina letu kutoka duniani;+ nawe utafanya nini kwa ajili ya jina lako kuu?”+

10 Naye Yehova akamwambia Yoshua: “Simama, wewe! Kwa nini unaanguka kifudifudi? 11 Israeli wametenda dhambi, nao wamevunja agano langu+ ambalo niliwaamuru; tena wamechukua sehemu ya vitu vilivyotengwa kwa ajili ya kuharibiwa,+ tena wameiba,+ tena wamevificha+ na kuvitia katikati ya vyombo vyao wenyewe.+ 12 Na wana wa Israeli hawataweza kusimama juu ya adui zao.+ Watawageuzia mgongo adui zao, kwa sababu wamekuwa kitu kilichotengwa kwa ajili ya kuharibiwa. Sitakuwa pamoja nanyi tena isipokuwa mharibu kutoka katikati yenu kitu kilichotengwa kwa ajili ya kuharibiwa.+ 13 Simama! Watakase watu,+ nawe useme, ‘Jitakaseni kesho, kwa maana Yehova Mungu wa Israeli amesema hivi: “Kitu kilichotengwa kwa ajili ya kuharibiwa kimo katikati yenu, Ee Israeli.+ Hamtaweza kusimama juu ya adui zenu mpaka mtakapoondoa katikati yenu kile kitu kilichotengwa kwa ajili ya kuharibiwa. 14 Nanyi mtakuja asubuhi, kabila kwa kabila, na itatukia kwamba kabila ambalo Yehova atalichagua+ litakaribia, familia kwa familia, na familia ambayo Yehova ataichagua itakaribia, nyumba kwa nyumba, na nyumba ambayo Yehova ataichagua itakaribia, mwanamume kwa mwanamume. 15 Na itatukia kwamba mtu atakayechaguliwa akiwa na kile kitu kilichotengwa kwa ajili ya kuharibiwa atateketezwa kwa moto,+ yeye na vyote vilivyo vyake, kwa sababu amevunja agano+ la Yehova na kwa sababu amefanya upumbavu wenye kufedhehesha katika Israeli.”’”+

16 Ndipo Yoshua akaamka asubuhi na mapema, akawaleta Israeli karibu, kabila kwa kabila, na kabila la Yuda likachaguliwa. 17 Kisha akaleta karibu familia za Yuda, naye akachagua familia ya Wazera,+ kisha akaleta karibu familia ya Wazera, mwanamume kwa mwanamume, na Zabdi akachaguliwa. 18 Mwishowe akaleta karibu nyumba yake, mwanamume kwa mwanamume, na Akani mwana wa Karmi, mwana wa Zabdi, mwana wa Zera, wa kabila la Yuda, akachaguliwa.+ 19 Ndipo Yoshua akamwambia Akani: “Tafadhali, mwanangu, mpe Yehova Mungu wa Israeli utukufu+ na uungame kwake,+ tafadhali niambie,+ Umefanya nini? Usinifiche+ jambo hili.”

20 Ndipo Akani akamjibu Yoshua na kusema: “Ni kweli—nimemtendea dhambi Yehova Mungu wa Israeli,+ nami nimefanya hivi na hivi. 21 Nilipoona+ katikati ya nyara vazi rasmi kutoka Shinari,+ lenye kupendeza, na shekeli 200 za fedha na kipande kimoja cha dhahabu, uzito wake ukiwa shekeli 50, ndipo nikavitamani+ vitu hivyo, halafu nikavichukua;+ na, tazama! vimefichwa chini ya udongo katikati ya hema langu na zile pesa chini yake.”+

22 Mara moja Yoshua akatuma wajumbe, wakakimbia kwenda hemani, na, tazama! vile vitu vilikuwa vimefichwa katika hema lake, na zile pesa chini yake. 23 Basi wakavichukua kutoka katikati ya lile hema, wakavileta kwa Yoshua na kwa wana wote wa Israeli na kuvimwaga mbele za Yehova. 24 Basi Yoshua, na Israeli wote pamoja naye, wakamchukua Akani+ mwana wa Zera na ile fedha na lile vazi rasmi na kile kipande cha dhahabu+ na wanawe na binti zake na ng’ombe zake na punda zake na kundi lake na hema lake na kila kitu kilichokuwa chake, wakawaleta katika nchi tambarare ya chini ya Akori.+ 25 Ndipo Yoshua akasema: “Kwa nini umeleta laana juu yetu?+ Leo hii Yehova ataleta laana juu yako.” Ndipo Israeli wote wakampiga kwa mawe,+ kisha wakawateketeza kwa moto.+ Kwa hiyo wakawapiga kwa mawe. 26 Nao wakaweka rundo kubwa la mawe juu yake, mpaka leo hii.+ Ndipo Yehova akaiacha hasira yake inayowaka.+ Ndiyo sababu jina la mahali hapo limeitwa Nchi Tambarare ya Chini ya Akori,+ mpaka leo hii.

8 Kisha Yehova akamwambia Yoshua: “Usiogope wala usiwe na hofu.+ Wachukue pamoja nawe watu wote wa vita kisha usimame, mwende Ai. Tazama, nimemtia mkononi mwako mfalme wa Ai na watu wake na jiji lake na nchi yake.+ 2 Nawe unapaswa kulitendea Ai na mfalme wake kama vile ulivyolitendea Yeriko na mfalme wake.+ Lakini mnaweza kupora nyara zake na wanyama wake wa kufugwa kwa ajili yenu wenyewe.+ Weka kikundi cha kulivizia jiji upande wake wa nyuma.”+

3 Basi Yoshua na watu wote wa vita+ wakasimama waende Ai, kisha Yoshua akachagua wanaume wenye nguvu+ 30,000, akawatuma wakati wa usiku. 4 Naye akawaamuru, akisema: “Angalieni, mtajificha na kulivizia+ jiji, upande wa nyuma wa jiji. Msiende mbali sana na jiji, nanyi nyote kaeni tayari. 5 Lakini mimi na watu wote walio pamoja nami, tutaenda karibu na jiji. Na itatukia kwamba, wakitoka nje kukutana nasi kama walivyofanya pale mwanzoni,+ ndipo sisi tutakapokimbia mbele yao. 6 Nao watatoka nje watufuate mpaka tutakapokuwa tumewavuta mbali na jiji hilo, kwa maana watasema, ‘Wanakimbia mbele yetu kama walivyofanya pale mwanzoni.’+ Nasi tutakimbia mbele yao. 7 Kisha ninyi mtasimama kutoka hapo mlipovizia, nanyi mtalikamata jiji; na Yehova Mungu wenu hakika atalitia jiji hilo mikononi mwenu.+ 8 Na itatukia kwamba mara tu mtakapokuwa mmelikamata jiji, mtaliteketeza jiji kwa moto.+ Mnapaswa kufanya kulingana na neno la Yehova. Angalieni, nimewaamuru ninyi.”+

9 Kisha Yoshua akawatuma, nao wakaenda mahali pa kuvizia, wakapiga kambi kati ya Betheli na Ai upande wa magharibi wa Ai, naye Yoshua akaendelea kukaa usiku huo katikati ya watu.

10 Ndipo Yoshua akaamka asubuhi na mapema,+ akawakagua watu, kisha akapanda kwenda Ai mbele ya watu, yeye pamoja na wanaume wazee wa Israeli. 11 Na watu wote wa vita+ waliokuwa pamoja naye wakaenda, wapate kukaribia na kuwa mbele ya jiji, nao wakaanza kupiga kambi upande wa kaskazini wa Ai, pakiwa na bonde kati yao na Ai. 12 Wakati huohuo akachukua wanaume elfu tano hivi, akawaweka kuvizia+ kati ya Betheli+ na Ai, upande wa magharibi wa jiji. 13 Basi watu wakaweka kambi kuu iliyokuwa upande wa kaskazini wa jiji+ na wale wa nyuma kabisa waliokuwa upande wa magharibi wa jiji,+ kisha Yoshua akaanza kwenda usiku huo katikati ya ile nchi tambarare ya chini.

14 Na ikawa kwamba, mara tu mfalme wa Ai alipoona hilo, wanaume wa jiji lile wakafanya haraka, wakaamka mapema, wakatoka nje wakutane kupigana na Israeli, yeye na watu wake wote, kwa wakati uliowekwa, mbele ya ile nchi tambarare ya jangwa. Lakini yeye hakujua kwamba palikuwa na waliomvizia upande wa nyuma wa jiji.+ 15 Wakati Yoshua na Israeli wote walipopigwa mbele yao,+ wakaanza kukimbia kupitia njia ya nyika.+ 16 Ndipo watu wote waliokuwa ndani ya jiji wakaitwa wawafuatilie, nao wakamfuatilia Yoshua na kuvutwa mbali na jiji.+ 17 Hakubaki mtu yeyote ndani ya Ai na Betheli ambaye hakufuatilia Israeli, hivyo wakaliacha jiji wazi kabisa, wakawafuatilia Israeli.

18 Sasa Yehova akamwambia Yoshua: “Nyoosha mkuki ulio mkononi mwako kuelekea Ai,+ kwa maana nitalitia mkononi mwako.”+ Basi Yoshua akaunyoosha mkuki uliokuwa mkononi mwake kuelekea jiji lile. 19 Na waliovizia wakasimama haraka kutoka mahali pao, nao wakaanza kukimbia mara tu aliponyoosha mkono wake, wakaingia ndani ya jiji na kulikamata.+ Kisha wakafanya haraka na kuliwasha moto jiji hilo.+

20 Ndipo watu wa Ai wakaanza kugeuka nyuma wakaona, na tazama, moshi wa jiji hilo ulikuwa unapaa juu mbinguni, na ndani yao haukubaki uwezo wowote wa kukimbia huku au huku. Kisha wale watu waliokuwa wakikimbilia nyikani wakawageukia wale waliokuwa wakiwafuatilia. 21 Na Yoshua na Israeli wote wakaona kwamba waliovizia+ walikuwa wamelikamata jiji hilo, na kwamba moshi wa jiji ulikuwa unapaa juu, kwa hiyo wakageuka, wakaanza kuwapiga na kuwaua watu wa Ai. 22 Na hao wengine wakatoka katika jiji kuja kukutana nao, hata wale wakawa katikati ya Israeli, hawa upande huu na hawa upande ule, nao wakawaua hata asibaki yeyote kati yao, mwenye kuokoka wala mwenye kupona.+ 23 Naye mfalme+ wa Ai wakamkamata akiwa hai, wakamleta karibu na Yoshua.

24 Na ikawa kwamba Israeli walipokuwa wakimaliza kuwaua wakaaji wote wa Ai uwanjani, katika nyika ambamo walikuwa wamewafuatilia, wote waliendelea kuanguka, kwa makali ya upanga mpaka walipokwisha. Kisha Israeli wote wakarudi Ai na kulipiga kwa makali ya upanga. 25 Na wote walioanguka siku hiyo, kuanzia mwanamume mpaka mwanamke, jumla yao ilikuwa kumi na mbili elfu, watu wote wa Ai. 26 Yoshua naye hakuurudisha nyuma mkono wake ambao alitumia kunyoosha ule mkuki+ mpaka alipokuwa amewaangamiza+ wakaaji wote wa Ai. 27 Ni wanyama wa kufugwa peke yao na nyara za jiji ndizo ambazo Israeli waliteka kwa ajili yao wenyewe, kulingana na neno la Yehova ambalo alikuwa amemwamuru Yoshua.+

28 Kisha Yoshua akateketeza Ai na kulifanya kuwa kilima kinachodumu mpaka wakati usio na kipimo,+ na kuwa ukiwa mpaka leo hii. 29 Naye akamtundika mfalme wa Ai+ juu ya mti mpaka jioni;+ na jua lilipokaribia kutua, Yoshua akatoa amri nao wakachukua maiti yake+ kutoka mtini na kuitupa kwenye mwingilio wa lango la jiji nao wakaweka rundo kubwa la mawe juu yake, mpaka leo hii.

30 Ndipo Yoshua akaanza kujenga madhabahu+ kwa Yehova Mungu wa Israeli, katika Mlima Ebali,+ 31 kama vile Musa mtumishi wa Yehova alivyokuwa amewaamuru wana wa Israeli, kama ilivyoandikwa katika kitabu cha sheria+ ya Musa: “Madhabahu ya mawe mazima, ambayo chombo cha chuma hakikutumiwa juu yake”;+ nao wakatoa juu yake matoleo ya kuteketezwa kwa Yehova na kutoa dhabihu za ushirika.+

32 Kisha akaandika hapo juu ya mawe nakala+ ya maandishi ya sheria ya Musa ambayo alikuwa ameandika mbele ya wana wa Israeli.+ 33 Na Israeli wote na wanaume wao wazee+ na maofisa na waamuzi wao walikuwa wamesimama upande huu wa Sanduku na upande ule mwingine mbele ya makuhani+ Walawi, waliochukua sanduku la agano la Yehova,+ mkaaji mgeni na mwenyeji+ vilevile, nusu yao walisimama mbele ya Mlima Gerizimu+ na nusu ile nyingine mbele ya Mlima Ebali,+ (kama vile Musa mtumishi wa Yehova alivyokuwa ameamuru,)+ ili kuwabariki+ watu wa Israeli kwanza. 34 Kisha akasoma kwa sauti maneno yote ya sheria,+ baraka+ na laana,+ kulingana na yote ambayo yameandikwa katika kitabu cha sheria. 35 Hakuna neno lolote kati ya yote ambayo Musa alikuwa ameamuru ambalo Yoshua hakusoma kwa sauti mbele ya kutaniko lote la Israeli,+ pamoja na wanawake+ na watoto wadogo+ na wakaaji wageni+ waliokuwa katikati yao.

9 Na ikawa kwamba mara tu wafalme wote+ waliokuwa ng’ambo ya Yordani iliyo katika eneo lenye milima na katika Shefela na kando ya pwani yote ya ile Bahari Kuu+ na mbele ya Lebanoni,+ Wahiti+ na Waamori, Wakanaani,+ Waperizi,+ Wahivi na Wayebusi,+ waliposikia habari hizo, 2 wakaanza kukusanyika pamoja ili kupigana vita na Yoshua na Israeli kwa kauli moja.+

3 Na wakaaji wa Gibeoni+ wakasikia mambo ambayo Yoshua alikuwa ametendea Yeriko+ na Ai.+ 4 Basi wao, kwa kupenda kwao wenyewe, wakatenda kwa werevu,+ wakajiwekea akiba ya vyakula na kuchukua magunia yaliyochakaa kwa ajili ya punda zao, na viriba vya divai vilivyochakaa, vilivyopasuka na kufungwa,+ 5 na viatu vilivyochakaa na kupigwa viraka miguuni mwao, wakavaa mavazi yaliyochakaa, na mkate wote wa vyakula vyao ukawa mkavu na wenye kuvunjika-vunjika. 6 Kisha wakaenda kwa Yoshua kambini katika Gilgali+ na kumwambia yeye na watu wa Israeli hivi: “Sisi tumetoka nchi ya mbali. Basi sasa fanyeni agano+ pamoja nasi.” 7 Ndipo watu wa Israeli wakawaambia hao Wahivi:+ “Labda mnakaa katika ujirani wetu. Basi tunawezaje kufanya agano pamoja nanyi?”+ 8 Nao wakamwambia Yoshua: “Sisi ni watumishi wako.”+

Kisha Yoshua akawaambia: “Ninyi ni nani, nanyi mnatoka wapi?” 9 Ndipo wakamwambia: “Watumishi wako wametoka nchi ya mbali sana+ kwa sababu ya jina+ la Yehova Mungu wako, kwa kuwa tumesikia sifa zake na mambo yote ambayo alitenda katika Misri,+ 10 na yote ambayo aliwatendea wale wafalme wawili wa Waamori waliokuwa ng’ambo ile nyingine ya Yordani, yaani, Sihoni+ mfalme wa Heshboni na Ogu+ mfalme wa Bashani, aliyekuwa katika Ashtarothi.+ 11 Basi wazee wetu na wakaaji wote wa nchi yetu wakatuambia hivi,+ ‘Chukueni chakula mikononi mwenu kwa ajili ya safari kisha mwende mkakutane nao, nanyi mtawaambia hivi: “Sisi ni watumishi wenu.+ Basi sasa fanyeni agano pamoja nasi.”’+ 12 Mkate wetu huu ulikuwa moto tulipouchukua kuwa chakula chetu kutoka katika nyumba zetu siku ile tulipoanza safari ya kuja hapa kwenu, na sasa, tazama! umekauka nao umekuwa wenye kuvunjika-vunjika.+ 13 Na hivi ndivyo viriba vya divai ambavyo tulivijaza vikiwa vipya, na tazama! vimepasuka,+ na mavazi haya na viatu vyetu, vimechakaa kwa sababu ya safari ya mbali sana.”

14 Ndipo watu hao wakachukua sehemu ya vyakula vyao, wala hawakuuliza habari kutoka katika kinywa cha Yehova.+ 15 Naye Yoshua akafanya amani nao,+ akafanya agano nao ili kuwaacha waishi, kwa hiyo wakuu+ wa kusanyiko wakawaapia.+

16 Na ikawa kwamba mwishoni mwa siku tatu, baada ya kufanya agano nao, wakapata kusikia kwamba walikuwa karibu nao, na kwamba walikuwa wakikaa katika ujirani wao. 17 Ndipo wana wa Israeli wakaondoka na kwenda katika majiji ya watu hao siku ya tatu, na majiji yao yalikuwa Gibeoni+ na Kefira+ na Beerothi+ na Kiriath-yearimu.+ 18 Nao wana wa Israeli hawakuwapiga, kwa sababu wakuu wa kusanyiko walikuwa wamewaapia+ kwa Yehova Mungu wa Israeli.+ Na kusanyiko lote likaanza kuwanung’unikia hao wakuu.+ 19 Kwa hiyo wakuu wote wakaliambia kusanyiko lote: “Sisi wenyewe tumewaapia kwa Yehova Mungu wa Israeli, na sasa hatuna ruhusa ya kuwadhuru.+ 20 Hili ndilo jambo tutakalowafanyia, kisha tuwaache waishi, ili hasira yoyote isitupate kwa sababu ya kile kiapo ambacho tumewaapia.”+ 21 Basi wakuu wakawaambia hivi: “Waacheni waishi, na wawe wakusanyaji wa kuni na watekaji wa maji kwa ajili ya kusanyiko lote,+ kama hao wakuu walivyowaahidi.”+

22 Basi sasa Yoshua akawaita na kuwaambia: “Kwa nini mlitufanyia ujanja, mkisema, ‘Tumetoka mbali sana na ninyi,’+ na kumbe mnakaa kati yetu?+ 23 Basi sasa ninyi ni watu waliolaaniwa,+ nanyi hamtaacha kamwe kuwa watumwa+ na wakusanyaji wa kuni na watekaji wa maji kwa ajili ya nyumba ya Mungu wangu.”+ 24 Ndipo wakamjibu Yoshua na kusema: “Kwa sababu watumishi wako waliambiwa waziwazi kwamba Yehova Mungu wako alikuwa amemwamuru Musa mtumishi wake awape ninyi nchi yote na kuwaangamiza wakaaji wote wa nchi kutoka mbele yenu,+ nasi tukaogopa sana kwa ajili ya nafsi zetu kwa sababu yenu.+ Kwa hiyo tukafanya jambo hili.+ 25 Na sasa tupo hapa, mkononi mwako. Basi kama unavyoona kuwa ni vema na sawa machoni pako kututendea, tutendee hivyo.”+ 26 Kwa hiyo akawatendea hivyo na kuwakomboa kutoka mkononi mwa wana wa Israeli, nao hawakuwaua.+ 27 Basi Yoshua akawafanya+ siku hiyo kuwa wakusanyaji wa kuni na watekaji wa maji kwa ajili ya kusanyiko+ na kwa ajili ya madhabahu ya Yehova, mpaka leo hii, mahali ambapo angechagua.+

10 Na ikawa kwamba mara tu Adoni-sedeki mfalme wa Yerusalemu aliposikia kwamba Yoshua ameteka Ai+ na kuliharibu,+ kwamba jinsi alivyofanya Yeriko+ na mfalme wake,+ ndivyo alivyofanya Ai na mfalme wake,+ na kwamba wakaaji wa Gibeoni walikuwa wamefanya amani na Israeli+ na kuendelea kukaa katikati yao, 2 akaogopa sana,+ kwa sababu Gibeoni lilikuwa jiji kubwa, kama moja la majiji ya kifalme, na kwa sababu lilikuwa kubwa kuliko Ai,+ na wanaume wake wote walikuwa wenye nguvu. 3 Basi Adoni-sedeki mfalme wa Yerusalemu+ akatuma ujumbe kwa Hohamu mfalme wa Hebroni+ na kwa Piramu mfalme wa Yarmuthi+ na kwa Yafia mfalme wa Lakishi+ na kwa Debiri mfalme wa Egloni,+ akisema, 4 “Pandeni mje kwangu, mnisaidie, tupige Gibeoni, kwa sababu wamefanya amani na Yoshua na wana wa Israeli.”+ 5 Ndipo wakakusanyika pamoja na kupanda, wafalme watano wa Waamori,+ mfalme wa Yerusalemu, mfalme wa Hebroni, mfalme wa Yarmuthi, mfalme wa Lakishi, mfalme wa Egloni, hao na kambi zao zote, nao wakaanza kupiga kambi juu ya Gibeoni na kupiga vita juu yake.

6 Ndipo watu wa Gibeoni wakatuma ujumbe kwa Yoshua huko Gilgali kambini,+ wakisema: “Usiulegeze mkono wako uwaache watumwa wako.+ Panda uje kwetu haraka, utuokoe na kutusaidia, kwa maana wafalme wote wa Waamori wanaokaa katika eneo lenye milima wamekusanyika pamoja kutupiga sisi.” 7 Basi Yoshua akapanda kutoka Gilgali, yeye na watu wote wa vita pamoja naye na mashujaa wote,+ wanaume wenye nguvu.+

8 Ndipo Yehova akamwambia Yoshua: “Usiwaogope,+ kwa maana nimewatia hao mkononi mwako.+ Hakuna mtu yeyote kati yao atakayesimama juu yako.”+ 9 Ndipo Yoshua akaja juu yao kwa ghafula. Alikuwa amepanda kutoka Gilgali usiku kucha. 10 Yehova naye akawavuruga mbele ya Israeli,+ nao wakaanza kuwaua kwa mauaji makuu katika Gibeoni,+ wakawafuatilia kwa njia ya mpando wa Beth-horoni, wakawaua mpaka Azeka+ na Makeda.+ 11 Na ikawa kwamba walipokuwa wanakimbia kutoka mbele ya Israeli, wakiwa kwenye mteremko wa Beth-horoni, Yehova akawatupia mawe+ makubwa kutoka mbinguni mpaka Azeka, nao wakafa. Wale waliokufa kutokana na hayo mawe ya mvua walikuwa wengi kuliko wale ambao wana wa Israeli waliwaua kwa upanga.

12 Ndipo Yoshua akaanza kusema na Yehova siku ile ambayo Yehova aliwatia Waamori mikononi mwa wana wa Israeli, naye akasema machoni pa Israeli:

“Ewe jua,+ simama tuli juu ya Gibeoni,+

Nawe mwezi, juu ya nchi tambarare ya chini ya Aiyaloni.”+

13 Basi jua likasimama tuli, mwezi nao ukasimama, mpaka taifa hilo lilipokuwa limelipiza kisasi juu ya adui zake.+ Je, habari hizo hazikuandikwa katika kitabu cha Yashari?+ Na jua likaendelea kusimama katikati ya mbingu nalo halikuharakisha kwenda kutua kwa karibu siku nzima.+ 14 Na hakuna siku ambayo imepata kuwa kama hiyo, wala kabla yake wala baada yake, kwa kuwa Yehova aliisikia sauti ya mwanadamu,+ kwa maana Yehova mwenyewe alikuwa akipigania Israeli.+

15 Baadaye Yoshua na Israeli wote pamoja naye wakarudi kambini huko Gilgali.+

16 Wakati huohuo wale wafalme watano wakakimbia,+ wakaenda kujificha katika pango huko Makeda.+ 17 Ndipo Yoshua akapata habari, ikisema: “Wale wafalme watano wamepatikana wakiwa wamejificha katika pango kule Makeda.”+ 18 Basi Yoshua akasema: “Viringisheni mawe makubwa katika kinywa cha pango hilo na kuweka watu juu ya pango hilo wawalinde. 19 Lakini ninyi msisimame. Wafuatilieni adui zenu, nanyi mwapige upande wa nyuma.+ Msiwaache waingie katika majiji yao, kwa kuwa Yehova Mungu wenu amewatia mikononi mwenu.”+

20 Na ikawa kwamba mara tu Yoshua na wana wa Israeli walipomaliza kuwaua kwa mauaji makubwa sana, mpaka wakakomeshwa,+ na wale waliobaki kati yao wakakimbia na kuingia katika majiji yenye ngome,+ 21 watu wote wakaanza kurudi kwa amani kambini, kwa Yoshua, katika Makeda. Hakuna mtu yeyote aliyeutoa ulimi wake kinyume cha wana wa Israeli.+ 22 Ndipo Yoshua akasema: “Fungueni kinywa cha pango, watoeni hawa wafalme watano kutoka ndani ya pango, mkawalete kwangu.” 23 Basi wakafanya hivyo, wakawatoa hao wafalme watano ndani ya pango, wakawaleta kwake, mfalme wa Yerusalemu,+ mfalme wa Hebroni,+ mfalme wa Yarmuthi, mfalme wa Lakishi,+ mfalme wa Egloni.+ 24 Na ikawa kwamba mara tu walipokuwa wamewaleta wafalme hao kwa Yoshua, Yoshua akawaita wanaume wote wa Israeli na kuwaambia viongozi wa wanaume wa vita waliokuwa wameenda pamoja naye: “Haya, sogeeni mbele. Wekeni nyayo za miguu yenu upande wa nyuma wa shingo za wafalme hawa.”+ Basi wakasogea mbele, wakaweka nyayo za miguu yao upande wa nyuma wa shingo zao.+ 25 Tena Yoshua akawaambia: “Msiogope wala msiingiwe na hofu.+ Iweni hodari na wenye nguvu, kwa maana hivi ndivyo Yehova atakavyowatendea adui zenu wote ambao mnapigana vita nao.”+

26 Kisha Yoshua akawapiga na kuwaua, akawatundika juu ya miti mitano, nao wakaendelea kuning’inia juu ya miti hiyo mpaka jioni.+ 27 Na ikawa kwamba Yoshua akatoa amri wakati wa kutua kwa jua, nao wakawashusha kutoka juu ya miti+ hiyo na kuwatupa ndani ya pango ambamo walikuwa wamejificha. Kisha wakaweka mawe makubwa katika kinywa cha pango hilo—mpaka leo hii.

28 Na Yoshua akateka Makeda+ siku hiyo, akalipiga kwa makali ya upanga. Naye akamwangamiza mfalme wake na kila nafsi iliyokuwamo ndani yake.+ Hakuacha mtu yeyote aokoke. Kwa hiyo akamtendea mfalme wa Makeda+ kama vile alivyomtendea mfalme wa Yeriko.

29 Kisha Yoshua na Israeli wote pamoja naye wakapita kutoka Makeda mpaka Libna, wakapiga vita juu ya Libna.+ 30 Basi Yehova akalitia jiji hilo na mfalme wake pia mkononi mwa Israeli, nao wakalipiga jiji hilo na kila nafsi iliyokuwa ndani yake kwa makali ya upanga. Hawakuacha mtu yeyote aokoke ndani yake. Kwa hiyo wakamtendea mfalme wake kama vile walivyomtendea mfalme wa Yeriko.+

31 Kisha Yoshua na Israeli wote pamoja naye wakapita kutoka Libna mpaka Lakishi,+ wakapiga kambi juu yake na kupiga vita juu yake. 32 Kwa hiyo Yehova akatia Lakishi mkononi mwa Israeli, nao wakaliteka siku ya pili, wakalipiga kwa makali ya upanga na pia kila nafsi iliyokuwa ndani yake,+ kulingana na yote ambayo walikuwa wamelitendea Libna.

33 Ndipo Horamu mfalme wa Gezeri+ akapanda kusaidia Lakishi. Basi Yoshua akampiga yeye na watu wake hata hakuacha mtu yeyote wake aokoke.+

34 Kisha Yoshua na Israeli wote wakapita kutoka Lakishi mpaka Egloni,+ wakapiga kambi juu yake na kupiga vita juu yake. 35 Nao wakaliteka siku hiyo na kuanza kulipiga kwa makali ya upanga, wakaangamiza siku hiyo kila nafsi iliyokuwa ndani yake, kulingana na yote ambayo walikuwa wamelitendea Lakishi.+

36 Kisha Yoshua na Israeli wote pamoja naye wakapanda kutoka Egloni mpaka Hebroni,+ wakaanza kupiga vita juu yake. 37 Nao wakaliteka, wakalipiga pamoja na mfalme wake na miji yake yote na kila nafsi iliyokuwa ndani yake kwa makali ya upanga. Hakuacha mtu yeyote aokoke, kulingana na yote aliyokuwa amelitendea Egloni. Kwa hiyo akaliangamiza+ pamoja na kila nafsi iliyokuwa ndani yake.

38 Mwishowe Yoshua na Israeli wote pamoja naye wakarudi Debiri,+ wakaanza kupiga vita juu yake. 39 Naye akaliteka pamoja na mfalme wake na miji yake yote, wakawapiga kwa makali ya upanga na kuangamiza+ kila nafsi iliyokuwa ndani yake. Hakuacha mtu yeyote aokoke.+ Kulingana na vile alivyolitendea Hebroni, ndivyo alivyolitendea Debiri na mfalme wake, na kama vile alivyolitendea Libna na mfalme wake.+

40 Na Yoshua akaanza kuipiga nchi yote ya eneo lenye milima+ na Negebu+ na Shefela+ na miteremko+ na wafalme wao wote. Hakuacha mtu yeyote aokoke,+ akaangamiza+ kila kitu kilichopumua, kama vile Yehova Mungu wa Israeli alivyokuwa ameamuru.+ 41 Naye Yoshua akawapiga kutoka Kadesh-barnea+ mpaka Gaza+ na nchi yote ya Gosheni+ kufika Gibeoni.+ 42 Na Yoshua akateka wafalme hao wote na nchi zao wakati mmoja,+ kwa kuwa ni Yehova Mungu wa Israeli aliyekuwa akipigania Israeli.+ 43 Baada ya hayo Yoshua na Israeli wote pamoja naye wakarudi kambini huko Gilgali.+

11 Na ikawa kwamba mara tu Yabini mfalme wa Hasori aliposikia habari hizo, akatuma ujumbe kwa Yobabu mfalme wa Madoni+ na kwa mfalme wa Shimroni na mfalme wa Akshafi,+ 2 na kwa wafalme waliokuwa upande wa kaskazini katika eneo lenye milima na katika nchi tambarare za jangwa upande wa kusini wa Kinerethi+ na katika Shefela+ na katika safu za milima ya Dori+ upande wa magharibi, 3 Wakanaani+ upande wa mashariki na magharibi, na Waamori+ na Wahiti+ na Waperizi+ na Wayebusi+ katika eneo lenye milima na Wahivi,+ pale chini ya Hermoni+ katika nchi ya Mispa.+ 4 Basi wakatoka, wao na kambi zao zote pamoja nao, hesabu kubwa sana ya watu kama chembe za mchanga ulio kando ya bahari kwa wingi,+ na farasi+ wengi sana na magari ya vita. 5 Ndipo wafalme hao wote wakakutana pamoja kwa mapatano, wakaja na kupiga kambi pamoja kando ya maji ya Meromu ili kupigana na Israeli.+

6 Ndipo Yehova akamwambia Yoshua: “Usiogope kwa sababu yao,+ kwa maana kesho karibu wakati kama huu nitawatoa wote kwa Israeli wakiwa wamechinjwa. Mtawalemaza farasi wao kwa kuwakata mishipa ya upande wa nyuma wa magoti,+ nayo magari yao mtayateketeza kwa moto.”+ 7 Na Yoshua na watu wote wa vita pamoja naye wakaja juu yao kwa ghafula kando ya maji ya Meromu, wakawaangukia. 8 Ndipo Yehova akawatia mkononi+ mwa Israeli, nao wakawapiga na kuwafuatilia mpaka Sidoni+ jiji lenye hesabu kubwa ya watu na Misrefoth-maimu+ na nchi tambarare ya bondeni ya Mispe+ upande wa mashariki; nao wakaendelea kuwapiga, hata asibaki yeyote kati yao mwenye kuokoka.+ 9 Kisha Yoshua akawatendea kama vile Yehova alivyokuwa amemwambia: akakata mishipa ya upande wa nyuma wa magoti ya farasi wao,+ nayo magari yao akayateketeza katika moto.+

10 Tena Yoshua akageuka wakati huo+ na kuteka Hasori;+ akampiga na kumuua mfalme wake kwa upanga,+ kwa sababu kabla ya wakati huo, Hasori lilikuwa ndilo kichwa cha falme hizo zote. 11 Nao wakaipiga kila nafsi iliyokuwa ndani yake kwa makali ya upanga, na kuwaangamiza.+ Hakuna kitu chochote kinachopumua ambacho kilibakia,+ naye akateketeza Hasori katika moto. 12 Na Yoshua akateka majiji yote ya wafalme hao, naye akawakamata wafalme wao wote, akawapiga kwa makali ya upanga.+ Akawaangamiza,+ kama vile Musa mtumishi wa Yehova alivyokuwa ameamuru.+ 13 Majiji ambayo Israeli hawakuteketeza ni yale yote yanayosimama juu ya vilima vyao peke yake, ila Yoshua aliteketeza jiji la Hasori tu. 14 Na wana wa Israeli wakapora kwa ajili yao wenyewe nyara zote za majiji hayo na wanyama wa kufugwa.+ Walipiga kwa makali ya upanga binadamu wote peke yao, mpaka walipokuwa wamewaangamiza.+ Hawakuacha yeyote anayepumua abaki.+ 15 Kama vile Yehova alivyokuwa amemwamuru Musa mtumishi wake, ndivyo Musa alivyomwamuru Yoshua,+ na ndivyo Yoshua alivyofanya. Hakuondoa hata neno moja kutoka kwa yote ambayo Yehova alikuwa amemwamuru Musa.+

16 Na Yoshua akachukua nchi hiyo yote, eneo lenye milima na Negebu+ yote na nchi yote ya Gosheni+ na Shefela+ na Araba+ na eneo lenye milima la Israeli na Shefela yake,+ 17 kutoka Mlima Halaki,+ unaopanda mpaka Seiri,+ na mpaka Baal-gadi+ katika nchi tambarare ya bondeni ya Lebanoni, pale chini ya Mlima Hermoni,+ naye akawakamata wafalme wao wote, akawapiga na kuwaua.+ 18 Yoshua alipiga vita na wafalme hao wote kwa siku nyingi. 19 Hakuna jiji lolote lililofanya amani na wana wa Israeli isipokuwa Wahivi+ wanaokaa Gibeoni.+ Majiji mengine yote waliyachukua kwa vita.+ 20 Kwa kuwa hiyo ndiyo iliyokuwa njia ya Yehova ya kutenda, kuacha mioyo yao iwe migumu+ ili watangaze vita juu ya Israeli, kusudi awaangamize, ili wasipate kibali,+ bali ili yeye apate kuwaangamiza, kama vile Yehova alivyokuwa amemwamuru Musa.+

21 Na zaidi ya hayo, Yoshua, wakati uleule, akaenda na kuwakatilia mbali Waanaki+ kutoka katika eneo lenye milima, kutoka Hebroni, kutoka Debiri, kutoka Anabu+ na kutoka katika eneo lote lenye milima la Yuda na kutoka katika eneo lote lenye milima la Israeli.+ Yoshua akawaangamiza+ pamoja na majiji yao. 22 Hakuna Waanaki wowote walioachwa katika nchi ya wana wa Israeli. Walibaki+ tu katika Gaza,+ katika Gathi+ na katika Ashdodi.+ 23 Basi Yoshua akaichukua nchi yote, kulingana na yote ambayo Yehova alikuwa amemwahidi Musa,+ kisha Yoshua akawapa Israeli iwe urithi wao kulingana na mafungu yao, kulingana na makabila yao.+ Na nchi haikusumbuliwa na vita tena.+

12 Basi hawa ndio wafalme wa nchi ambao wana wa Israeli waliwashinda, na kuimiliki nchi yao ng’ambo ya Yordani upande wa mapambazuko ya jua,+ kutoka bonde la mto la Arnoni+ hadi Mlima Hermoni+ na Araba+ yote upande wa mashariki: 2 Sihoni+ mfalme wa Waamori, aliyekaa katika Heshboni,+ akitawala kutoka Aroeri,+ lililokuwa kwenye ukingo wa bonde la mto la Arnoni,+ na katikati ya bonde la mto, na nusu ya Gileadi hadi bonde la mto la Yaboki,+ mpaka wa wana wa Amoni, 3 na Araba+ hadi bahari ya Kinerethi+ kuelekea mashariki hadi bahari ya Araba, yaani, Bahari ya Chumvi,+ upande wa mashariki kuelekea Beth-yeshimothi,+ na kuelekea kusini chini ya miteremko ya Pisga.+

4 Na eneo la Ogu+ mfalme wa Bashani, lile lililobaki la Warefaimu,+ waliokaa katika Ashtarothi+ na Edrei,+ 5 na waliotawala katika Mlima Hermoni+ na katika Saleka na katika Bashani+ yote, hadi mpaka wa Wageshuri+ na Wamaakathi,+ na nusu ya Gileadi, hadi katika eneo la Sihoni+ mfalme wa Heshboni.+

6 Musa mtumishi wa Yehova na wana wa Israeli ndio waliowashinda,+ kisha Musa mtumishi wa Yehova akawapa Warubeni+ na Wagadi+ na nusu ya kabila la Manase+ iwe urithi wao.

7 Na hawa ndio wafalme wa nchi ambao Yoshua na wana wa Israeli waliwashinda ng’ambo ya Yordani kuelekea magharibi, kuanzia Baal-gadi+ katika nchi tambarare ya bondeni ya Lebanoni+ hadi Mlima Halaki,+ unaopanda hadi Seiri,+ kisha Yoshua akawapa makabila ya Israeli iwe urithi wao kulingana na mafungu yao,+ 8 katika eneo lenye milima na katika Shefela na katika Araba na kwenye miteremko na katika nyika na katika Negebu+—Wahiti, Waamori+ na Wakanaani, Waperizi, Wahivi na Wayebusi:+

 9 Mfalme wa Yeriko,+ mmoja; mfalme wa Ai,+ jiji lililokuwa kando ya Betheli, mmoja;

10 mfalme wa Yerusalemu,+ mmoja; mfalme wa Hebroni,+ mmoja;

11 mfalme wa Yarmuthi,+ mmoja; mfalme wa Lakishi,+ mmoja;

12 mfalme wa Egloni,+ mmoja; mfalme wa Gezeri,+ mmoja;

13 mfalme wa Debiri,+ mmoja; mfalme wa Gederi, mmoja;

14 mfalme wa Horma, mmoja; mfalme wa Aradi, mmoja;

15 mfalme wa Libna,+ mmoja; mfalme wa Adulamu, mmoja;

16 mfalme wa Makeda,+ mmoja; mfalme wa Betheli,+ mmoja;

17 mfalme wa Tapua, mmoja; mfalme wa Heferi,+ mmoja;

18 mfalme wa Afeki, mmoja; mfalme wa Lasharoni, mmoja;

19 mfalme wa Madoni,+ mmoja; mfalme wa Hasori,+ mmoja;

20 mfalme wa Shimron-meroni, mmoja; mfalme wa Akshafi,+ mmoja;

21 mfalme wa Taanaki, mmoja; mfalme wa Megido,+ mmoja;

22 mfalme wa Kedeshi, mmoja; mfalme wa Yokneamu+ katika Karmeli, mmoja;

23 mfalme wa Dori katika safu ya milima ya Dori,+ mmoja; mfalme wa Goiimu katika Gilgali, mmoja;

24 mfalme wa Tirsa, mmoja; wafalme wote walikuwa 31.+

13 Basi Yoshua alikuwa mzee, amesonga katika miaka.+ Kwa hiyo Yehova akamwambia: “Wewe mwenyewe umezeeka na kusonga katika miaka, na sehemu kubwa ya nchi bado haijamilikiwa.+ 2 Hii ndiyo nchi ambayo bado imebaki:+ maeneo yote ya Wafilisti+ na Wageshuri+ wote 3 (kutoka kile kijito cha Nile kilichoko mbele ya Misri hadi kwenye mpaka wa Ekroni upande wa kaskazini,+ ilikuwa ikihesabiwa kuwa ni ya Wakanaani);+ wakuu watano+ wa muungano wa Wafilisti, Wagaza+ na Waashdodi,+ Waashkeloni,+ Wagathi+ na Waekroni;+ na Waavimu.+ 4 Upande wa kusini, nchi yote ya Wakanaani; na Meara, ambayo ni ya Wasidoni,+ hadi Afeki, hadi mpaka wa Waamori; 5 na nchi ya Wagebali+ na Lebanoni yote upande wa mapambazuko ya jua, kuanzia Baal-gadi+ ulio chini ya Mlima Hermoni hadi maingilio ya Hamathi;+ 6 wakaaji wote wa eneo lenye milima, kutoka Lebanoni+ hadi Misrefoth-maimu,+ Wasidoni+ wote; mimi mwenyewe nitawanyang’anya nchi na kuwafukuza mbele ya wana wa Israeli.+ Uwawezeshe wana wa Israeli kuirithi, kama vile ambavyo nimekuamuru.+ 7 Na sasa igawe nchi hii iwe urithi kwa yale makabila tisa na kwa ile nusu ya kabila la Manase.”+

8 Na pamoja na ile nusu nyingine ya kabila, Warubeni na Wagadi walichukua urithi wao ambao Musa aliwapa ng’ambo ya Yordani iliyo upande wa mashariki, kama vile Musa mtumishi wa Yehova alivyokuwa amewapa,+ 9 kutoka Aroeri,+ lililo kwenye ukingo wa bonde la mto la Arnoni,+ na lile jiji lililo katikati ya hilo bonde la mto, na nchi yote tambarare ya juu ya Medeba+ hadi Diboni;+ 10 na majiji yote ya Sihoni mfalme wa Waamori, aliyetawala katika Heshboni, hadi kwenye mpaka wa wana wa Amoni;+ 11 na Gileadi na eneo la Wageshuri+ na Wamaakathi na Mlima Hermoni+ wote na Bashani+ yote hadi Saleka;+ 12 ufalme wote wa Ogu+ katika Bashani, aliyetawala katika Ashtarothi na katika Edrei+—yeye ndiye aliyebaki kati ya mabaki ya Warefaimu+—kwa kuwa Musa aliwapiga na kuwanyang’anya nchi na kuwafukuza.+ 13 Na wana wa Israeli hawakuwafukuza+ Wageshuri na Wamaakathi katika nchi, bali Geshuri+ na Maakathi huendelea kukaa katikati ya Israeli mpaka leo hii.

14 Kabila la Walawi peke yake ndilo ambalo hakulipatia urithi.+ Matoleo ya Yehova Mungu wa Israeli yaliyotolewa kwa njia ya moto+ ndiyo urithi wao,+ kama vile ambavyo amewaahidi.+

15 Ndipo Musa akalipatia zawadi kabila la wana wa Rubeni kulingana na familia zao, 16 na eneo lao likawa kutoka Aroeri,+ lililo kwenye ukingo wa bonde la mto la Arnoni, na lile jiji lililo katikati ya bonde la mto, na nchi yote tambarare ya juu, karibu na Medeba;+ 17 Heshboni+ na miji yake yote+ iliyo katika nchi tambarare ya juu, Diboni+ na Bamoth-baali+ na Beth-baal-meoni,+ 18 na Yahazi+ na Kedemothi+ na Mefaathi,+ 19 na Kiriathaimu+ na Sibma+ na Sereth-shahari katika mlima wa nchi tambarare ya chini, 20 na Beth-peori na miteremko ya Pisga+ na Beth-yeshimothi,+ 21 na majiji yote ya nchi tambarare ya juu+ na ufalme wote wa Sihoni mfalme wa Waamori, aliyetawala katika Heshboni,+ na ambaye Musa alimpiga na kumuua,+ pamoja na wakuu wa Midiani, Evi na Rekemu na Suri na Huru na Reba,+ watawala wadogo wa Sihoni, waliokuwa wakikaa katika nchi hiyo. 22 Na Balaamu mwana wa Beori,+ yule mwaguzi,+ wana wa Israeli wakamuua kwa upanga pamoja na watu waliouawa. 23 Na mpaka wa wana wa Rubeni ukawa Yordani; na eneo hilo likawa urithi wa wana wa Rubeni+ kulingana na familia zao, pamoja na majiji na makao yake.

24 Tena, Musa akalipatia zawadi kabila la Gadi, wana wa Gadi kulingana na familia zao,+ 25 na eneo lao likawa Yazeri+ na majiji yote ya Gileadi+ na nusu ya nchi ya wana wa Amoni+ hadi Aroeri,+ lililo mbele ya Raba;+ 26 na kutoka Heshboni+ hadi Ramath-mispe na Betonimu na kutoka Mahanaimu+ hadi mpaka wa Debiri;+ 27 na katika nchi tambarare ya chini Beth-haramu+ na Beth-nimra+ na Sukothi+ na Safoni, sehemu iliyobaki ya ufalme wa Sihoni mfalme wa Heshboni,+ mto Yordani ukawa mpaka hadi mwisho wa bahari ya Kinerethi+ ng’ambo ya pili ya Yordani upande wa mashariki. 28 Huo ndio uliokuwa urithi wa wana wa Gadi+ kulingana na familia zao, pamoja na majiji na makao yake.

29 Na zaidi, Musa akalipatia zawadi nusu ya kabila la Manase, nayo ikawa ya ile nusu ya kabila la wana wa Manase kulingana na familia zao.+ 30 Na eneo lao likawa kutoka Mahanaimu+ na Bashani yote, ufalme wote wa Ogu mfalme wa Bashani,+ na vijiji vyote vya mahema vya Yairi+ vilivyo katika Bashani, miji 60. 31 Na nusu ya Gileadi, na Ashtarothi+ na Edrei,+ majiji ya ufalme wa Ogu katika Bashani, ikaenda kwa wana wa Makiri+ mwana wa Manase, kwa nusu ya wana wa Makiri kulingana na familia zao.

32 Musa aliwapa maeneo hayo kuwa urithi, katika nchi tambarare za jangwa la Moabu ng’ambo ya Yordani, huko Yeriko, upande wa mashariki.+

33 Lakini Musa hakuwapa urithi kabila la Walawi.+ Yehova Mungu wa Israeli ndiye urithi wao, kama vile ambavyo amewaahidi.+

14 Basi hili ndilo fungu la urithi ambalo wana wa Israeli walichukua katika nchi ya Kanaani,+ ambalo Eleazari kuhani na Yoshua mwana wa Nuni na vichwa vya baba za makabila ya wana wa Israeli waliwapa kuwa urithi.+ 2 Urithi wao ulikuwa kwa kura,+ kama vile Yehova alivyokuwa ameamuru yale makabila tisa na ile nusu ya kabila kupitia kwa Musa.+ 3 Kwa maana Musa alikuwa ametoa urithi wa yale makabila mawili na wa ile nusu ya kabila ng’ambo ile nyingine ya Yordani;+ naye hakuwapa Walawi urithi katikati yao.+ 4 Kwa maana wana wa Yosefu walikuwa wamekuwa makabila mawili,+ Manase+ na Efraimu;+ nao hawakuwa wamewapa Walawi fungu katika nchi, isipokuwa majiji+ ya kukaa na viwanja vyao vya malisho kwa ajili ya mifugo yao na mali zao.+ 5 Wana wa Israeli walifanya vile ambavyo Yehova alikuwa amemwamuru Musa; nao wakaanza kuigawanya nchi.

6 Ndipo wana wa Yuda wakamkaribia Yoshua katika Gilgali,+ na Kalebu+ mwana wa Yefune Mkenizi,+ akamwambia: “Wewe unajua vema lile neno ambalo Yehova alimwambia+ Musa yule mtu wa Mungu wa kweli+ juu yangu na juu yako kule Kadesh-barnea.+ 7 Nilikuwa na umri wa miaka 40 wakati Musa mtumishi wa Yehova aliponituma kutoka Kadesh-barnea kwenda kuipeleleza nchi,+ nami nikamletea habari kama vile ilivyokuwa ndani ya moyo wangu.+ 8 Na ndugu zangu walioenda pamoja nami wakaifanya mioyo ya watu iyeyuke;+ lakini mimi nilimfuata kikamilifu Yehova Mungu wangu.+ 9 Basi Musa akaapa siku hiyo, akisema, ‘Nchi ambayo mguu wako umekanyaga+ itakuwa yako na ya wana wako, iwe urithi mpaka wakati usio na kipimo, kwa kuwa umemfuata Yehova Mungu wangu kikamilifu.’+ 10 Basi sasa, tazama, Yehova amenihifadhi hai,+ kama vile alivyoahidi,+ hii miaka 45 tangu Yehova alipotoa ahadi hii kwa Musa, Israeli walipotembea nyikani.+ Na sasa, tazama, leo nina umri wa miaka 85. 11 Lakini bado mimi leo nina nguvu kama vile nilivyokuwa siku ile ambayo Musa alinituma.+ Kama nguvu zangu zilivyokuwa wakati huo, ndivyo nguvu zangu zilivyo sasa kwa ajili ya vita, za kutoka nje na za kuingia ndani.+ 12 Na sasa nipe basi eneo hili lenye milima ambalo Yehova aliahidi siku hiyo,+ kwa kuwa wewe mwenyewe ulisikia siku hiyo kwamba huko kulikuwa na Waanaki+ na majiji makubwa yenye ngome.+ Huenda Yehova atakuwa pamoja nami,+ nami nitawanyang’anya nchi na kuwafukuza, kama vile Yehova alivyoahidi.”+

13 Basi Yoshua akambariki, akampa Kalebu mwana wa Yefune, Hebroni kuwa urithi wake.+ 14 Ndiyo sababu mpaka leo hii Hebroni limekuwa urithi wa Kalebu mwana wa Yefune Mkenizi, kwa maana alimfuata Yehova Mungu wa Israeli kikamilifu.+ 15 Jina la Hebroni hapo mwanzoni lilikuwa Kiriath-arba+ (huyo Arba+ alikuwa mwanamume mkuu kati ya Waanaki). Na nchi haikusumbuliwa na vita tena.+

15 Na kura+ ya kabila la wana wa Yuda kulingana na familia zao ikawa hadi kwenye mpaka wa Edomu,+ nyika ya Zini,+ hadi Negebu+ mwisho wake wa upande wa kusini. 2 Na mpaka wao wa kusini ukawa kutoka mwisho wa Bahari ya Chumvi,+ kuanzia ghuba inayoelekea kusini. 3 Nao ukaelekea upande wa kusini kuelekea kwenye mpando wa Akrabimu+ na kuvuka hadi Zini+ na kupanda kutoka kusini hadi Kadesh-barnea+ na kuvuka hadi Hezroni na kupanda hadi Adari na kuzunguka hadi Karka. 4 Nao ukaendelea hadi Asimoni+ na kwenda hadi kwenye bonde la mto la Misri;+ na mwisho wa mpaka huo ukawa kwenye bahari. Huo ukawa ndio mpaka wao wa upande wa kusini.

5 Na mpaka wa upande wa mashariki ulikuwa Bahari ya Chumvi hadi mwisho wa Yordani, na mpaka kwenye pembe ya upande wa kaskazini ulikuwa katika ghuba ya bahari, katika sehemu ya mwisho ya Yordani.+ 6 Na mpaka huo ukapanda hadi Beth-hogla+ na kuvuka upande wa kaskazini wa Beth-araba,+ na mpaka huo ukapanda hadi kwenye jiwe la Bohani+ mwana wa Rubeni. 7 Na mpaka huo ukapanda hadi Debiri katika nchi tambarare ya chini ya Akori+ na kugeuka kuelekea kaskazini hadi Gilgali,+ lililo mbele ya mpando wa Adumimu, ambao uko upande wa kusini wa bonde la mto; na mpaka huo ukaendelea hadi kwenye maji ya En-shemeshi,+ na mwisho wake ukawa En-rogeli.+ 8 Na mpaka huo ukapanda hadi bonde la mwana wa Hinomu+ kwenye mteremko wa Myebusi+ upande wa kusini, yaani, Yerusalemu;+ na mpaka huo ukapanda hadi kwenye kilele cha mlima unaoelekeana na bonde la Hinomu upande wa magharibi, ambao uko mwisho wa nchi tambarare ya chini ya Refaimu+ upande wa kaskazini. 9 Kisha mpaka huo ulitiwa alama kutoka kilele cha mlima hadi kwenye bubujiko la maji ya Neftoa,+ ukaenda kwenye majiji ya Mlima Efroni; na mpaka huo ulitiwa alama hadi Baala,+ yaani, Kiriath-yearimu.+ 10 Na mpaka huo ukazunguka kutoka Baala kuelekea upande wa magharibi hadi Mlima Seiri ukaendelea hadi kwenye mteremko wa Mlima Yearimu upande wa kaskazini, yaani, Kesaloni; nao ukashuka hadi Beth-shemeshi+ na kuendelea hadi Timna.+ 11 Na mpaka huo ukaenda hadi kwenye mteremko wa Ekroni+ upande wa kaskazini, na mpaka huo ulitiwa alama hadi Shikeroni na kuendelea hadi Mlima Baala na kwenda hadi Yabneeli; na mwisho wa mpaka huo ukawa kwenye bahari.

12 Na mpaka wa upande wa magharibi ulikuwa kwenye Bahari Kuu+ na nchi iliyo kando yake. Huu ndio uliokuwa mpaka wa wana wa Yuda kuzunguka pande zote kulingana na familia zao.

13 Naye akampa Kalebu+ mwana wa Yefune fungu katikati ya wana wa Yuda kama Yehova alivyomwamuru Yoshua, yaani, Kiriath-arba (huyo Arba alikuwa baba ya Anaki), yaani, Hebroni.+ 14 Basi Kalebu akawafukuza kutoka huko wale wana watatu wa Anaki,+ yaani, Sheshai+ na Ahimani na Talmai,+ waliozaliwa kwa Anaki.+ 15 Kisha akapanda kutoka huko hadi kwa wakaaji wa Debiri.+ (Jina la Debiri hapo mwanzoni lilikuwa Kiriath-seferi.)+ 16 Ndipo Kalebu akasema: “Yeyote atakayepiga Kiriath-seferi na kuliteka, hakika nitampa Aksa+ binti yangu awe mke wake.” 17 Ndipo Othnieli+ mwana wa Kenasi,+ ndugu ya Kalebu, akaliteka. Basi akampa Aksa+ binti yake awe mke wake. 18 Na ikawa kwamba mwanamke huyo alipokuwa akienda nyumbani, aliendelea kumchochea mume wake aombe shamba kutoka kwa baba-mkwe wake. Ndipo mwanamke huyo akapiga makofi akiwa juu ya punda. Naye Kalebu akamwambia: “Unataka nini?”+ 19 Naye akasema: “Unipe baraka, kwa maana umenipa sehemu ya shamba upande wa kusini, nawe unipe Guloth-maimu.” Basi akampa Gulothi ya Juu na Gulothi ya Chini.+

20 Huo ndio uliokuwa urithi+ wa kabila la wana wa Yuda+ kulingana na familia zao.

21 Na majiji katika sehemu ya mwisho ya kabila la wana wa Yuda kuelekea mpaka wa Edomu+ upande wa kusini yalikuwa ni Kabzeeli+ na Ederi na Yaguri, 22 na Kina na Dimona na Adada, 23 na Kedeshi na Hasori na Ithnani, 24 Zifu na Telemu+ na Bealothi, 25 na Hasor-hadata na Kerioth-hesroni, yaani, Hasori, 26 Amamu na Shema na Molada,+ 27 na Hasar-gada na Heshmoni na Beth-peleti,+ 28 na Hasar-shuali+ na Beer-sheba+ na Biziothia, 29 Baala+ na Iimu na Esemu,+ 30 na Eltoladi na Kesili na Horma,+ 31 na Siklagi+ na Madmana na Sansana, 32 na Lebaothi na Shilhimu na Aini+ na Rimoni;+ majiji yote yalikuwa 29, pamoja na makao yake.

33 Katika Shefela+ kulikuwa na Eshtaoli+ na Sora+ na Ashna, 34 na Zanoa+ na En-ganimu, Tapua na Enamu, 35 Yarmuthi+ na Adulamu,+ Soko+ na Azeka,+ 36 na Shaaraimu+ na Adithaimu na Gedera na Gederothaimu; majiji kumi na manne na makao yake.

37 Senani na Hadasha na Migdal-gadi, 38 na Dileani na Mispe na Yoktheeli, 39 Lakishi+ na Boskathi+ na Egloni,+ 40 na Kaboni na Lahmamu na Kitilishi, 41 na Gederothi, Beth-dagoni na Naama na Makeda;+ majiji kumi na sita na makao yake.

42 Libna+ na Etheri+ na Ashani, 43 na Ifta na Ashna na Nesibu, 44 na Keila+ na Akzibu+ na Maresha;+ majiji tisa na makao yake.

45 Ekroni+ na miji yake ya kandokando na makao yake. 46 Kutoka Ekroni kuelekea magharibi yote ambayo iko kandokando ya Ashdodi na makao yake.

47 Ashdodi,+ miji yake ya kandokando na makao yake; Gaza,+ miji yake ya kandokando na makao yake, hadi kwenye bonde la mto la Misri, na ile Bahari Kuu na eneo jirani.+

48 Na katika eneo lenye milima, Shamiri na Yatiri+ na Soko, 49 na Dana na Kiriath-sana, yaani, Debiri, 50 na Anabu na Eshtemo+ na Animu, 51 na Gosheni+ na Holoni na Gilo;+ majiji kumi na moja na makao yake.

52 Arabu na Duma na Eshani, 53 na Yanimu na Beth-tapua na Afeka, 54 na Humta na Kiriath-arba, yaani, Hebroni,+ na Siori; majiji tisa na makao yake.

55 Maoni,+ Karmeli na Zifu+ na Yuta, 56 na Yezreeli na Yokdeamu na Zanoa, 57 Kayini, Gibea na Timna;+ majiji kumi na makao yake.

58 Halhuli, Beth-suri na Gedori, 59 na Maarathi na Beth-anothi na Eltekoni; majiji sita na makao yake.

60 Kiriath-baali,+ yaani, Kiriath-yearimu,+ na Raba; majiji mawili na makao yake.

61 Katika nyika, Beth-araba,+ Midini na Sekaka, 62 na Nibshani na Jiji la Chumvi na En-gedi;+ majiji sita na makao yake.

63 Lakini wale Wayebusi+ waliokuwa wakikaa katika Yerusalemu,+ wana wa Yuda hawakuweza kuwafukuza;+ basi hao Wayebusi wanaendelea kukaa pamoja na wana wa Yuda katika Yerusalemu mpaka leo hii.

16 Na kura+ ya wana wa Yosefu+ ikawa kutoka Yordani+ huko Yeriko hadi kwenye maji ya Yeriko upande wa mashariki, nyika inayopanda kutoka Yeriko hadi katika eneo lenye milima la Betheli.+ 2 Na ikatoka Betheli, iliyokuwa ya Luzi+ na kwenda hadi kwenye mpaka wa Waarki+ huko Atarothi, 3 nayo ikashuka kwenda magharibi hadi kwenye mpaka wa Wayafleti hadi kwenye mpaka wa Beth-horoni+ ya Chini na Gezeri,+ na mwisho wake ukawa kwenye bahari.+

4 Na wana wa Yosefu,+ Manase na Efraimu,+ wakaanza kuimiliki nchi.+ 5 Na mpaka wa wana wa Efraimu kulingana na familia zao ulikuwa, ndiyo, mpaka wa urithi wao upande wa mashariki ulikuwa Ataroth-adari,+ hadi Beth-horoni ya Juu;+ 6 na mpaka huo ukaenda hadi baharini. Mikmethathi+ ilikuwa upande wa kaskazini, na mpaka huo ukazunguka upande wa mashariki hadi Taanath-shilo, ukaenda upande wa mashariki hadi Yanoa. 7 Nao ukashuka kutoka Yanoa hadi Atarothi na Naara ukafika Yeriko+ na kwenda hadi Yordani. 8 Kutoka Tapua+ mpaka huo ukaendelea upande wa magharibi hadi kwenye bonde la mto la Kana,+ na mwisho wake ukawa kwenye bahari.+ Huo ndio urithi wa kabila la wana wa Efraimu kulingana na familia zao. 9 Na wana wa Efraimu walikuwa na majiji yaliyozungukwa+ katikati ya urithi wa wana wa Manase, majiji yote na makao yake.

10 Nao hawakuwafukuza Wakanaani+ waliokuwa wakikaa katika Gezeri,+ na Wakanaani hao huendelea kukaa katikati ya Efraimu mpaka leo hii,+ nao wakawa watumishi wa kazi ya kulazimishwa.+

17 Na kura+ ikawa kwa ajili ya kabila la Manase,+ kwa sababu alikuwa mzaliwa wa kwanza wa Yosefu,+ kwa ajili ya Makiri+ mzaliwa wa kwanza wa Manase, baba ya Gileadi,+ kwa sababu alikuwa mtu wa vita;+ na Gileadi+ na Bashani zikawa zake. 2 Na kura ikawa kwa wana wa Manase waliobaki kulingana na familia zao, kwa wana wa Abiezeri+ na wana wa Heleki+ na wana wa Asrieli na wana wa Shekemu+ na wana wa Heferi na wana wa Shemida.+ Hao walikuwa wana wa Manase mwana wa Yosefu, wanaume kulingana na familia zao. 3 Lakini Selofehadi+ mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, hakuwa na wana, ila mabinti, na haya ndiyo yaliyokuwa majina ya hao mabinti zake: Mala na Noa, Hogla, Milka na Tirsa.+ 4 Basi wakaja mbele ya Eleazari+ kuhani na Yoshua mwana wa Nuni na wakuu, wakisema: “Yehova ndiye aliyemwamuru Musa atupe sisi urithi katikati ya ndugu zetu.”+ Basi akawapa urithi katikati ya ndugu za baba yao kwa agizo la Yehova.+

5 Na kulikuwa na mafungu kumi kwa ajili ya Manase mbali na nchi ya Gileadi na Bashani, zilizokuwa ng’ambo ile nyingine ya Yordani;+ 6 kwa kuwa binti za Manase walipata urithi katikati ya wanawe; na nchi ya Gileadi ikawa mali ya wana wa Manase waliobaki.

7 Na mpaka wa Manase ukawa kutoka Asheri hadi Mikmethathi,+ eneo lililo mbele ya Shekemu,+ na mpaka huo ukasonga kuelekea upande wa kuume kwa wakaaji wa En-Tapua. 8 Hiyo nchi ya Tapua+ ikawa ya Manase, lakini Tapua katika mpaka wa Manase ilikuwa ya wana wa Efraimu. 9 Na mpaka huo ukashuka hadi kwenye bonde la mto la Kana, kuelekea kusini hadi kwenye bonde la mto la majiji haya+ ya Efraimu katikati ya majiji ya Manase, na mpaka wa Manase ulikuwa upande wa kaskazini wa bonde la mto, na mwisho wake ukawa kwenye bahari.+ 10 Upande wa kusini ulikuwa ni wa Efraimu na upande wa kaskazini ulikuwa ni wa Manase, na bahari ikawa ndiyo mpaka wake;+ nao upande wa kaskazini wanafika Asheri na upande wa mashariki wanafika Isakari.

11 Na Manase,+ katika Isakari na katika Asheri, wakawa na Beth-sheani+ na miji yake ya kandokando na Ibleamu+ na miji yake ya kandokando na wakaaji wa Dori+ na miji yake ya kandokando na wakaaji wa En-dori+ na miji yake ya kandokando na wakaaji wa Taanaki+ na miji yake ya kandokando na wakaaji wa Megido+ na miji yake ya kandokando, vilele vitatu.

12 Na wana wa Manase hawakuweza kuyamiliki majiji hayo,+ bali Wakanaani waliendelea kukaa katika nchi hiyo.+ 13 Na ikawa kwamba wakati wana wa Israeli walipokuwa wamepata nguvu,+ wakawaweka Wakanaani wafanye kazi ya kulazimishwa,+ wala hawakuwafukuza kikamilifu.+

14 Na ndipo wana wa Yosefu wakasema na Yoshua, wakamwambia: “Kwa nini umenipa kura+ moja na fungu moja kuwa urithi wangu, ingawa mimi nina watu wengi sana kwa kuwa Yehova amenibariki mpaka sasa?”+ 15 Ndipo Yoshua akawaambia: “Ikiwa ninyi ni watu wengi sana, nendeni msituni, mjikatie huko katika nchi ya Waperizi+ na Warefaimu,+ kwa sababu eneo lenye milima+ la Efraimu limekuwa jembamba mno kwenu.” 16 Kisha wana wa Yosefu wakasema: “Eneo hilo lenye milima halitutoshi, na kuna magari ya vita+ yenye miundu ya chuma kati ya Wakanaani wote wanaokaa katika nchi tambarare ya chini, wale walio katika Beth-sheani+ na miji yake ya kandokando na vilevile wale walio katika nchi tambarare ya chini ya Yezreeli.”+ 17 Kwa hiyo Yoshua akaiambia hivi nyumba ya Yosefu, Efraimu na Manase: “Ninyi ni watu wengi sana, nanyi mna nguvu nyingi.+ Hampaswi kupata kura moja,+ 18 lakini hilo eneo lenye milima linapaswa kuwa lenu.+ Kwa kuwa ni msitu, ukateni, nalo liwe ndilo mpaka wa mwisho kwa ajili yenu. Kwa kuwa mnapaswa kuwafukuza Wakanaani, ijapokuwa wana magari ya vita yenye miundu ya chuma nao wana nguvu.”+

18 Ndipo kusanyiko lote la wana wa Israeli likakutanika Shilo,+ nao wakaweka huko lile hema la mkutano,+ kwa maana sasa nchi ilikuwa imetiishwa mbele yao.+ 2 Lakini kati ya wana wa Israeli kulikuwa na wale ambao bado hawakuwa wamegawiwa urithi wao, yaani, makabila saba. 3 Kwa hiyo Yoshua akawaambia wana wa Israeli: “Mtakuwa wazembe mpaka wakati gani, msiingie kuimiliki nchi+ ambayo Yehova Mungu wa mababu zenu amewapa ninyi?+ 4 Jichagulieni wanaume watatu wa kila kabila, nami niwatume, wasimame na kutembea katika nchi na kuandika vipimo vyake vya ramani kulingana na urithi wao, kisha waje kwangu.+ 5 Nao waigawanye kati yao wenyewe iwe mafungu saba.+ Yuda ataendelea kusimama katika eneo lake upande wa kusini,+ na nyumba ya Yosefu wataendelea kusimama katika eneo lao upande wa kaskazini.+ 6 Nanyi kwa upande wenu, mtaandika vipimo vya ramani vya nchi katika mafungu saba, nanyi mtayaleta kwangu hapa, nami nitapiga kura+ hapa kwa ajili yenu mbele za Yehova Mungu wetu. 7 Kwa maana Walawi hawana fungu lolote katikati yenu,+ kwa kuwa ukuhani wa Yehova ndio urithi wao;+ na Gadi na Rubeni+ na nusu ya kabila la Manase+ wamechukua urithi wao ng’ambo ya Yordani upande wa mashariki, ambao Musa mtumishi wa Yehova amewapa.”+

8 Ndipo watu hao wakasimama ili waende, kisha Yoshua akawaamuru+ wale waliokuwa wakienda kuandika vipimo vya ramani vya nchi, akisema: “Nendeni, mtembee katika nchi na kuandika vipimo vyake vya ramani kisha mrudi kwangu, na hapa ndipo nitakapopiga kura+ kwa ajili yenu mbele za Yehova katika Shilo.”+ 9 Basi watu hao wakaenda, wakapita katikati ya nchi na kuandika vipimo vyake vya ramani+ ndani ya kitabu kulingana na majiji katika mafungu saba. Kisha wakamjia Yoshua kambini huko Shilo, 10 ndipo Yoshua akapiga kura kwa ajili yao katika Shilo mbele za Yehova.+ Basi Yoshua akawagawanyia wana wa Israeli nchi katika mafungu yao.+

11 Ndipo ilitokea kura+ ya kabila la wana wa Benyamini+ kulingana na familia zao, na eneo la kura yao likawa ni kati ya wana wa Yuda+ na wana wa Yosefu.+ 12 Na mpaka wao ukawa katika pembe ya kaskazini kutoka Yordani, na mpaka huo ukapanda hadi kwenye mteremko wa Yeriko+ upande wa kaskazini na kupanda kwenye mlima upande wa magharibi, na mwisho wake ukawa katika nyika ya Beth-aveni.+ 13 Kisha mpaka huo ukaendelea kutoka hapo hadi Luzi,+ kwenye mteremko wa kusini wa Luzi, yaani, Betheli;+ na mpaka huo ukashuka hadi Ataroth-adari+ juu ya mlima ulioko upande wa kusini wa Beth-horoni ya Chini.+ 14 Na mpaka huo ukatiwa alama na kuzunguka upande wa magharibi kuelekea kusini kutoka katika mlima unaoelekeana na Beth-horoni upande wa kusini; na mwisho wake ukawa katika Kiriath-baali, yaani, Kiriath-yearimu,+ jiji la wana wa Yuda. Huo ndio upande wa magharibi.

15 Na upande wa kusini ulikuwa ni kutoka mwisho wa Kiriath-yearimu, na mpaka huo ukaelekea upande wa magharibi na kuelekea kwenye bubujiko la maji ya Neftoa.+ 16 Na mpaka huo ukashuka kuelekea mwisho wa mlima unaoelekeana na bonde la mwana wa Hinomu,+ ambalo limo katika nchi tambarare ya chini ya Refaimu+ upande wa kaskazini, nao ukashuka katika bonde la Hinomu, kwenye mteremko wa Myebusi+ upande wa kusini, nao ukashuka hadi En-rogeli.+ 17 Nao ukatiwa alama kuelekea kaskazini na kwenda hadi En-shemeshi na kwenda hadi Gelilothi, eneo lililo mbele ya mpando wa Adumimu;+ nao ukashuka kuelekea kwenye jiwe+ la Bohani+ mwana wa Rubeni. 18 Kisha ukaendelea hadi mteremko wa kaskazini mbele ya Araba, nao ukashuka hadi Araba. 19 Na mpaka huo ukaendelea hadi mteremko wa kaskazini wa Beth-hogla,+ na mwisho wake (wa mpaka) ukawa katika ghuba ya kaskazini ya Bahari ya Chumvi+ kwenye mwisho wa upande wa kusini wa Yordani. Huo ndio uliokuwa mpaka wa upande wa kusini. 20 Na mto Yordani ukawa ndio mpaka wake upande wa mashariki. Huo ndio uliokuwa urithi wa wana wa Benyamini kulingana na familia zao, kulingana na mipaka yake kuzunguka pande zote.

21 Na majiji ya kabila la wana wa Benyamini kulingana na familia zao yalikuwa ni Yeriko+ na Beth-hogla na Emek-kesisi, 22 na Beth-araba+ na Semaraimu na Betheli,+ 23 na Avimu na Para na Ofra,+ 24 na Kefar-amoni na Ofni na Geba;+ majiji kumi na mawili na makao yake.

25 Gibeoni+ na Rama na Beerothi, 26 na Mispe+ na Kefira+ na Mosa, 27 na Rekemu na Irpeeli na Tarala, 28 na Zela,+ Ha-elefu na Yebusi, yaani, Yerusalemu,+ Gibea+ na Kiriathi; majiji kumi na manne na makao yake.

Huo ndio uliokuwa urithi wa wana wa Benyamini kulingana na familia zao.+

19 Kisha kura+ ya pili ilitokea kwa ajili ya Simeoni,+ kwa ajili ya kabila la wana wa Simeoni kulingana na familia zao. Na urithi wao ukawa katikati ya urithi wa wana wa Yuda.+ 2 Nao katika urithi wao wakawa na Beer-sheba+ pamoja na Sheba, na Molada,+ 3 na Hasar-shuali+ na Bala na Esemu,+ 4 na Eltoladi+ na Bethuli na Horma, 5 na Siklagi+ na Beth-markabothi na Hasar-susa,+ 6 na Beth-lebaothi+ na Sharuheni; majiji kumi na matatu na makao yake. 7 Aini,+ Rimoni+ na Etheri na Ashani;+ majiji manne na makao yake, 8 na makao yote yaliyokuwa pande zote kuzunguka majiji hayo mpaka kufika Baalath-beeri,+ Rama+ jiji la upande wa kusini. Huo ndio uliokuwa urithi wa kabila la wana wa Simeoni kulingana na familia zao. 9 Urithi wa wana wa Simeoni ulitoka katika fungu la wana wa Yuda, kwa sababu fungu la wana wa Yuda lilikuwa kubwa mno kwao.+ Basi wana wa Simeoni wakapata miliki katikati ya urithi wao.+

10 Kisha kura+ ya tatu ilikuwa ni kwa ajili ya wana wa Zabuloni+ kulingana na familia zao, na mpaka wa urithi wao ulifika hadi Saridi. 11 Na mpaka wao ukapanda upande wa magharibi pia ukafika hadi Mareali na kufika hadi Dabeshethi na kufika hadi bonde la mto ambalo liko mbele ya Yokneamu.+ 12 Nao ukarudi kutoka Saridi kuelekea mashariki upande wa mapambazuko ya jua kwenda hadi kwenye mpaka wa Kisloth-tabori nao ukaendelea hadi Daberathi+ na kupanda hadi Yafia. 13 Na kutoka hapo ukaelekea mashariki upande wa mapambazuko ya jua hadi Gath-heferi,+ hadi Eth-kazini, ukaenda hadi Rimoni ukatiwa alama hadi Nea. 14 Na mpaka huo ukalizunguka upande wa kaskazini hadi Hanathoni, na miisho yake ilifika kwenye bonde la Iftah-eli, 15 na Katathi na Nahalali na Shimroni+ na Idala na Bethlehemu;+ majiji kumi na mawili na makao yake. 16 Huo ndio uliokuwa urithi+ wa wana wa Zabuloni kulingana na familia zao.+ Hayo ndiyo yaliyokuwa majiji na makao yake.

17 Kura ya nne ilitokea kwa ajili ya Isakari,+ kwa ajili ya wana wa Isakari kulingana na familia zao. 18 Na mpaka wao ukafika hadi Yezreeli+ na Kesulothi na Shunemu,+ 19 na Hafaraimu na Shioni na Anaharathi, 20 na Rabithi na Kishioni na Ebesi, 21 na Remethi na En-ganimu+ na En-hada na Beth-pasesi. 22 Na mpaka huo ukafika hadi Tabori+ na Shahasuma na Beth-shemeshi, na miisho ya mpaka wao ilifika kwenye Yordani; majiji kumi na sita na makao yake. 23 Huo ndio uliokuwa urithi wa kabila la wana wa Isakari kulingana na familia zao,+ majiji na makao yake.

24 Ndipo kura+ ya tano ilitokea kwa ajili ya kabila la wana wa Asheri+ kulingana na familia zao. 25 Na mpaka wao ukawa ni Helkathi+ na Hali na Beteni na Akshafi,+ 26 na Alameleki na Amadi na Mishali.+ Nao ukafika upande wa magharibi hadi Karmeli+ hadi Shihor-libnathi, 27 nao ukarudi upande wa mapambazuko ya jua kuelekea Beth-dagoni, ukafika hadi Zabuloni+ na bonde la Iftah-eli upande wa kaskazini, hadi Beth-emeki na Neieli, ukaenda hadi Kabuli upande wa kushoto, 28 na hadi Ebroni na Rehobu na Hamoni na Kana hadi kufika Sidoni+ jiji lenye watu wengi. 29 Na mpaka huo ukarudi hadi Rama kufika hadi jiji lenye ngome la Tiro.+ Na mpaka huo ukarudi hadi Hosa, na miisho yake ilifika kwenye bahari katika eneo la Akzibu,+ 30 na Uma na Afeki+ na Rehobu;+ majiji 22 na makao yake. 31 Huo ndio uliokuwa urithi wa kabila la wana wa Asheri kulingana na familia zao.+ Hayo ndiyo yaliyokuwa majiji na makao yake.

32 Kura+ ya sita ilikuwa kwa ajili ya wana wa Naftali,+ kwa ajili ya wana wa Naftali kulingana na familia zao. 33 Na mpaka wao ukawa kutoka Helefu, kutoka kwenye ule mti mkubwa katika Saananimu,+ na Adami-nekebu na Yabneeli kufika hadi Lakumu; na miisho yake ilifika kwenye Yordani. 34 Na mpaka huo ukarudi kuelekea magharibi hadi Aznoth-tabori na kutoka hapo ukaenda hadi Hukkoki ukafika hadi Zabuloni+ upande wa kusini, na hadi Asheri+ ulifika upande wa magharibi na hadi Yuda+ kwenye Yordani upande wa mapambazuko ya jua. 35 Na majiji yenye ngome yalikuwa ni Sidimu, Seri na Hamathi,+ Rakathi na Kinerethi,+ 36 na Adama na Rama na Hasori,+ 37 na Kedeshi+ na Edrei na En-hasori, 38 na Yironi na Migdal-eli, Horemu na Beth-anathi na Beth-shemeshi;+ majiji kumi na tisa na makao yake. 39 Huo ndio uliokuwa urithi+ wa kabila la wana wa Naftali kulingana na familia zao,+ majiji na makao yake.

40 Kura+ ya saba ilitokea kwa ajili ya kabila la wana wa Dani+ kulingana na familia zao. 41 Na mpaka wa urithi wao ukawa ni Sora+ na Eshtaoli na Ir-shemeshi, 42 na Shaalabini+ na Aiyaloni+ na Ithla, 43 na Eloni na Timna+ na Ekroni,+ 44 na Elteke na Gibethoni+ na Baalathi,+ 45 na Yehudi na Bene-beraki na Gath-rimoni,+ 46 na Me-yarkoni na Rakoni, mpaka ukiwa mbele ya Yopa.+ 47 Na eneo la wana wa Dani lilifanya wafinyane mno.+ Nao wana wa Dani wakapanda na kupiga vita juu ya Leshemu+ na kuliteka, wakalipiga kwa makali ya upanga. Ndipo wakalimiliki na kukaa ndani yake, nao wakaliita Leshemu jina Dani, kulingana na jina la Dani babu yao.+ 48 Huo ndio uliokuwa urithi wa kabila la wana wa Dani kulingana na familia zao. Hayo ndiyo yaliyokuwa majiji na makao yake.

49 Hivyo wakamaliza kuigawanya nchi kuwa miliki kulingana na maeneo yake. Kisha wana wa Israeli wakampa urithi Yoshua mwana wa Nuni katikati yao. 50 Kwa agizo la Yehova walimpa jiji ambalo aliomba,+ yaani, Timnath-sera,+ katika eneo lenye milima la Efraimu; naye akalijenga jiji hilo na kukaa ndani yake.

51 Huo ndio uliokuwa urithi ambao Eleazari kuhani na Yoshua mwana wa Nuni na vichwa vya upande wa baba vya makabila ya wana wa Israeli waligawanya+ kuwa miliki kwa njia ya kura katika Shilo+ mbele za Yehova, kwenye mwingilio wa hema la mkutano.+ Basi wakaacha kuigawanya nchi.

20 Ndipo Yehova akasema na Yoshua, akamwambia: 2 “Sema na wana wa Israeli, uwaambie, ‘Mjipe wenyewe majiji ya makimbilio+ ambayo niliwaambia habari zake kupitia Musa, 3 ili muuaji+ anayepiga nafsi na kuiua bila kukusudia, bila kujua, akimbilie humo; nayo yatakuwa kwenu makimbilio kutoka kwa mlipiza-kisasi cha damu.+ 4 Naye atakimbilia+ moja la majiji hayo na kusimama hapo kwenye mwingilio wa lango+ la jiji na kusema maneno yake masikioni mwa wanaume wazee+ wa jiji hilo; nao watampokea kwao ndani ya jiji na kumpa mahali, akae pamoja nao. 5 Na mlipiza-kisasi cha damu akimfuatilia, basi wao hawapaswi kumtia muuaji huyo mkononi mwake;+ kwa maana alimpiga akamuua mwenzake bila kujua, wala hakuwa akimchukia hapo zamani.+ 6 Naye atakaa ndani ya jiji hilo mpaka atakaposimama mbele ya kusanyiko kwa ajili ya hukumu,+ mpaka kifo cha kuhani mkuu+ atakayekuwa katika cheo siku hizo. Ndipo muuaji huyo ataweza kurudi,+ naye ataingia katika jiji lake na katika nyumba yake, ndani ya jiji ambalo alikuwa amelikimbia.’”

7 Basi wakayapa hali ya utakatifu majiji ya Kedeshi+ katika Galilaya katika eneo lenye milima la Naftali, na Shekemu+ katika eneo lenye milima la Efraimu, na Kiriath-arba,+ yaani, Hebroni, katika eneo lenye milima la Yuda. 8 Na katika eneo la Yordani, kule Yeriko, upande wa mashariki wakatoa Beseri+ nyikani kwenye nchi tambarare ya juu kutoka katika kabila la Rubeni,+ na Ramothi+ katika Gileadi kutoka katika kabila la Gadi, na Golani+ katika Bashani kutoka katika kabila la Manase.

9 Hayo yakawa majiji yaliyochaguliwa kwa ajili ya wana wote wa Israeli na kwa ajili ya mkaaji mgeni anayekaa akiwa mgeni katikati yao, ili mtu yeyote anayepiga nafsi na kuiua bila kukusudia akimbilie humo,+ asife mkononi mwa mlipiza-kisasi cha damu mpaka atakaposimama mbele ya kusanyiko.+

21 Basi vichwa vya upande wa baba vya Walawi wakamkaribia Eleazari+ kuhani na Yoshua+ mwana wa Nuni na vichwa vya upande wa baba vya makabila ya wana wa Israeli, 2 kisha wakasema nao huko Shilo+ katika nchi ya Kanaani, wakiwaambia: “Yehova alitoa amri kupitia Musa kwamba sisi tupewe majiji ya kukaa, pamoja na viwanja vyake vya malisho kwa ajili ya wanyama wetu wa kufugwa.”+ 3 Basi wana wa Israeli wakawapa Walawi,+ kwa agizo la Yehova, majiji hayo na viwanja vyake vya malisho kutoka katika urithi wao.+

4 Ndipo kura ikatoka kwa ajili ya familia za Wakohathi,+ na wana wa Haruni kuhani, waliokuwa kati ya Walawi, wakawa na majiji kumi na matatu, yaliyochukuliwa kwa kura kutoka katika kabila la Yuda+ na kutoka katika kabila la Wasimeoni+ na kutoka katika kabila la Benyamini.+

5 Na wana waliobaki wa Kohathi+ walipata kwa kura majiji kumi kutoka katika familia za kabila la Efraimu+ na kutoka katika kabila la Dani+ na katika nusu ya kabila la Manase.+

6 Na kwa ajili ya wana wa Gershoni+ kulikuwa na majiji kumi na matatu kwa kura kutoka katika familia za kabila la Isakari+ na kutoka katika kabila la Asheri+ na kutoka katika kabila la Naftali+ na kutoka katika nusu ya kabila la Manase katika Bashani.+

7 Kwa ajili ya wana wa Merari+ kulingana na familia zao kulikuwa na majiji kumi na mawili kutoka katika kabila la Rubeni+ na kutoka katika kabila la Gadi+ na kutoka katika kabila la Zabuloni.+

8 Hivyo wana wa Israeli wakawapa Walawi majiji hayo na viwanja vyake vya malisho+ kwa kura+ kama Yehova alivyokuwa ametoa amri kupitia kwa Musa.+

9 Basi kutoka katika kabila la wana wa Yuda na katika kabila la wana wa Simeoni wakatoa majiji haya yaliyotajwa kwa majina,+ 10 nayo yakawa ya wana wa Haruni kutoka katika familia za Wakohathi wa wana wa Lawi, kwa kuwa kura ya kwanza ilikuwa yao.+ 11 Basi wakawapa Kiriath-arba+ (huyo Arba alikuwa baba ya Anaki),+ yaani, jiji la Hebroni,+ katika eneo lenye milima la Yuda,+ na viwanja vyake vya malisho kuzunguka pande zote; 12 na shamba la jiji hilo na makao yake wakampa Kalebu mwana wa Yefune kuwa miliki yake.+

13 Nao waliwapa wana wa Haruni kuhani jiji la makimbilio+ kwa ajili ya muuaji,+ yaani, Hebroni,+ na kiwanja chake cha malisho, pia Libna+ na kiwanja chake cha malisho, 14 na Yatiri+ na kiwanja chake cha malisho, na Eshtemoa+ na kiwanja chake cha malisho, 15 na Holoni+ na kiwanja chake cha malisho, na Debiri+ na kiwanja chake cha malisho, 16 na Aini+ na kiwanja chake cha malisho, na Yuta+ na kiwanja chake cha malisho, Beth-shemeshi+ na kiwanja chake cha malisho; majiji tisa yalichukuliwa kutoka katika makabila hayo mawili.

17 Na kutoka katika kabila la Benyamini, Gibeoni+ na kiwanja chake cha malisho, Geba+ na kiwanja chake cha malisho, 18 Anathothi+ na kiwanja chake cha malisho, na Almoni+ na kiwanja chake cha malisho; majiji manne.

19 Majiji yote ya wana wa Haruni,+ makuhani, yalikuwa majiji kumi na matatu na viwanja vyake vya malisho.+

20 Na kwa ajili ya familia za wana wa Kohathi, Walawi waliobaki kutoka kwa wana wa Kohathi, kwa kura yao kukawa na majiji katika kabila la Efraimu.+ 21 Basi wakawapa jiji la makimbilio+ kwa ajili ya muuaji,+ yaani, jiji la Shekemu,+ na kiwanja chake cha malisho+ katika eneo lenye milima la Efraimu, na Gezeri+ na kiwanja chake cha malisho, 22 na Kibsaimu+ na kiwanja chake cha malisho, na Beth-horoni+ na kiwanja chake cha malisho; majiji manne.

23 Na kutoka katika kabila la Dani, Elteke na kiwanja chake cha malisho, Gibethoni+ na kiwanja chake cha malisho, 24 Aiyaloni+ na kiwanja chake cha malisho, Gath-rimoni+ na kiwanja chake cha malisho; majiji manne.

25 Na kutoka katika nusu ya kabila la Manase, Taanaki+ na kiwanja chake cha malisho, na Gath-rimoni na kiwanja chake cha malisho; majiji mawili.

26 Majiji yote pamoja na viwanja vyake vya malisho ya familia za wana wa Kohathi waliobaki yalikuwa majiji kumi.

27 Na kwa ajili ya wana wa Gershoni,+ wa familia za Walawi, kulikuwa kutoka katika nusu ya kabila la Manase+ jiji la makimbilio kwa ajili ya muuaji, yaani, jiji la Golani,+ katika Bashani, na kiwanja chake cha malisho, na Beeshtera+ na kiwanja chake cha malisho; majiji mawili.

28 Na kutoka katika kabila la Isakari,+ Kishioni+ na kiwanja chake cha malisho, Daberathi+ na kiwanja chake cha malisho, 29 Yarmuthi+ na kiwanja chake cha malisho, En-ganimu+ na kiwanja chake cha malisho; majiji manne.

30 Na kutoka katika kabila la Asheri,+ Mishali+ na kiwanja chake cha malisho, Abdoni+ na kiwanja chake cha malisho, 31 Helkathi+ na kiwanja chake cha malisho, na Rehobu+ na kiwanja chake cha malisho; majiji manne.

32 Na kutoka katika kabila la Naftali,+ jiji la makimbilio+ kwa ajili ya muuaji,+ yaani, jiji la Kedeshi+ katika Galilaya, na kiwanja chake cha malisho, na Hamoth-dori+ na kiwanja chake cha malisho, na Kartani na kiwanja chake cha malisho; majiji matatu.

33 Majiji yote ya Wagershoni kulingana na familia zao yalikuwa majiji kumi na matatu na viwanja vyake vya malisho.

34 Na familia za wana wa Merari,+ Walawi waliobaki, kutoka katika kabila la Zabuloni+ walikuwa na Yokneamu+ na kiwanja chake cha malisho, Karta na kiwanja chake cha malisho, 35 Dimna+ na kiwanja chake cha malisho, Nahalali+ na kiwanja chake cha malisho; majiji manne.

36 Na kutoka katika kabila la Rubeni,+ Beseri+ na kiwanja chake cha malisho, na Yahazi+ na kiwanja chake cha malisho, 37 Kedemothi+ na kiwanja chake cha malisho, na Mefaathi+ na kiwanja chake cha malisho; majiji manne.

38 Na kutoka katika kabila la Gadi,+ jiji la makimbilio kwa ajili ya muuaji, yaani, jiji la Ramothi katika Gileadi,+ na kiwanja chake cha malisho, na Mahanaimu+ na kiwanja chake cha malisho, 39 Heshboni+ na kiwanja chake cha malisho, Yazeri+ na kiwanja chake cha malisho; majiji yote yalikuwa ni manne.

40 Majiji yote yaliyokuja kuwa ya wana wa Merari+ kulingana na familia zao, waliobaki kutoka kwa familia za Walawi, yalikuwa, kulingana na kura yao, majiji kumi na mawili.

41 Majiji yote ya Walawi katikati ya miliki ya wana wa Israeli yalikuwa ni majiji 48+ pamoja na viwanja vyake vya malisho.+ 42 Majiji hayo yakaja kuwa kila moja ni jiji pamoja na kiwanja chake cha malisho kulizunguka pande zote—ikawa hivyo kwa hayo majiji yote.+

43 Basi Yehova akawapa Israeli nchi yote ambayo alikuwa ameapa kuwapa mababu zao,+ nao wakaimiliki+ na kukaa ndani yake. 44 Tena Yehova akawapa pumziko+ kuwazunguka pande zote, kulingana na kila kitu ambacho alikuwa amewaapia+ mababu zao, wala hakuna mmoja kati ya adui zao wote aliyesimama mbele yao.+ Yehova aliwatia adui zao wote mkononi mwao.+ 45 Hakuna ahadi hata moja iliyokosa kutimia katika ahadi zote nzuri ambazo Yehova alikuwa ameipa nyumba ya Israeli; mambo yote yalitimia.+

22 Ndipo wakati huo Yoshua akawaita Warubeni na Wagadi na nusu ya kabila la Manase+ 2 naye akawaambia: “Ninyi kwa upande wenu mmetimiza mambo yote ambayo Musa mtumishi wa Yehova aliwaamuru,+ nanyi mmeitii sauti yangu katika mambo yote ambayo nimewaamuru.+ 3 Hamkuwaacha ndugu zenu muda wa hizi siku nyingi+ mpaka leo hii, nanyi mmeshika wajibu wa amri ya Yehova Mungu wenu.+ 4 Na sasa Yehova Mungu wenu amewapa ndugu zenu pumziko, kama vile alivyowaahidi.+ Basi sasa rudini, mwende zenu mahemani mwenu katika nchi ya miliki yenu, ambayo Musa mtumishi wa Yehova aliwapa ng’ambo ile nyingine ya Yordani.+ 5 Ila tu muwe waangalifu sana katika kutimiza amri+ na sheria ambazo Musa mtumishi wa Yehova aliwaamuru ninyi, kwa kumpenda Yehova Mungu wenu+ na kwa kutembea katika njia zake zote+ na kwa kushika amri zake+ na kwa kushikamana naye+ na kwa kumtumikia+ kwa moyo wenu wote+ na kwa nafsi yenu yote.”+

6 Basi Yoshua akawabariki+ na kuwaacha waende zao ili wapate kwenda kwa mahema yao. 7 Na Musa alikuwa ametoa zawadi ya urithi kwa nusu ya kabila la Manase katika Bashani,+ na kwa ile nusu nyingine Yoshua alitoa zawadi ya urithi pamoja na ndugu zao ng’ambo ile nyingine ya Yordani upande wa magharibi.+ Basi, pia, Yoshua alipowaacha waende zao kwa mahema yao, akawabariki. 8 Naye akawaambia: “Rudini katika mahema yenu mkiwa na utajiri mwingi pamoja na mifugo mingi sana, pamoja na fedha na dhahabu na shaba na chuma na mavazi kwa wingi sana.+ Chukueni fungu lenu la nyara+ za adui zenu pamoja na ndugu zenu.”

9 Kisha wana wa Rubeni na wana wa Gadi na nusu ya kabila la Manase wakarudi na kwenda zao kutoka kwa wale wana wengine wa Israeli, kutoka Shilo, lililo katika nchi ya Kanaani, ili waende katika nchi ya Gileadi,+ katika nchi ya miliki yao ambamo walikuwa wamepewa makao kwa agizo la Yehova kupitia Musa.+ 10 Walipofika katika maeneo ya Yordani yaliyokuwa katika nchi ya Kanaani, ndipo wana wa Rubeni na wana wa Gadi na nusu ya kabila la Manase wakajenga huko madhabahu kando ya Yordani, madhabahu+ kubwa yenye kuonekana wazi. 11 Baadaye wale wana wengine wa Israeli wakasikia+ ikisemwa: “Tazama! Wana wa Rubeni na wana wa Gadi na nusu ya kabila la Manase wamejenga madhabahu katika mpaka wa nchi ya Kanaani katika maeneo ya Yordani upande ulio miliki ya wana wa Israeli.” 12 Wana wa Israeli waliposikia habari hizo, kusanyiko zima la wana wa Israeli+ wakakutanishwa katika Shilo+ ili waende kuwachukulia hatua ya kijeshi.+

13 Ndipo wana wa Israeli wakamtuma+ Finehasi+ mwana wa Eleazari kuhani kwa wana wa Rubeni na wana wa Gadi na nusu ya kabila la Manase katika nchi ya Gileadi, 14 na wakuu kumi pamoja naye, mkuu mmoja kwa ajili ya kila nyumba ya ukoo wa upande wa baba ya makabila yote ya Israeli, na kila mmoja wao alikuwa ni mkuu wa nyumba ya baba zao katika maelfu ya Israeli.+ 15 Baada ya muda wakaja kwa wana wa Rubeni na wana wa Gadi na nusu ya kabila la Manase katika nchi ya Gileadi, wakaanza kuwaambia,+ wakisema:

16 “Kusanyiko lote la Yehova+ limesema hivi, ‘Mmefanya tendo gani hili la kukosa uaminifu+ juu ya Mungu wa Israeli kwa kugeuka+ nyuma msimfuate Yehova leo, mkajijengea madhabahu,+ ili kumwasi Yehova leo? 17 Je, lile kosa la Peori+ lilikuwa dogo mno kwetu, ambalo hatujajitakasa katika hilo mpaka leo hii, ingawa pigo lilikuja juu ya kusanyiko la Yehova?+ 18 Ninyi—ninyi mnageuka leo msimfuate Yehova; na itatukia kwamba ninyi, kwa upande wenu, mkimwasi Yehova leo, ndipo kesho atakuwa na ghadhabu juu ya kusanyiko lote la Israeli.+ 19 Basi sasa ikiwa kweli hiyo nchi iliyo miliki yenu ni najisi,+ vukeni mje katika nchi iliyo miliki ya Yehova+ mahali ambapo maskani ya Yehova imekaa,+ mkae katikati yetu; nanyi msimwasi Yehova wala msitufanye sisi tuasi kwa ninyi kujijengea madhabahu zaidi ya ile madhabahu ya Yehova Mungu wetu.+ 20 Je, Akani+ mwana wa Zera siye aliyefanya tendo la kukosa uaminifu kuhusiana na kile kitu kilichotengwa kwa ajili ya kuharibiwa, na je, hasira haikuja juu ya kusanyiko lote la Israeli?+ Wala yeye siye mtu peke yake aliyekufa katika kosa lake.’”+

21 Ndipo wana wa Rubeni na wana wa Gadi na nusu ya kabila la Manase wakajibu+ na kusema na vichwa vya maelfu ya Israeli:+ 22 “Mwenye Uwezo,+ Mungu,+ Yehova, Mwenye Uwezo, Mungu, Yehova,+ yeye anajua,+ na Israeli pia atajua.+ Ikiwa ni kwa uasi+ na ikiwa ni kwa kukosa uaminifu kwa Yehova,+ usituokoe leo hii. 23 Kama ilikuwa ni kujijengea madhabahu ili tugeuke tusimfuate Yehova, na kama tulitaka kutoa matoleo ya kuteketezwa na matoleo ya nafaka juu yake,+ na kama tulitaka kutoa dhabihu za ushirika juu yake, Yehova mwenyewe atachunguza;+ 24 au kama tulifanya hivyo kutokana na hangaiko juu ya jambo lingine, tukisema, ‘Siku fulani, wakati ujao, wana wenu watawaambia wana wetu: “Je, ninyi mna nini na Yehova Mungu wa Israeli? 25 Na kuna mpaka ambao Yehova ameweka kati yetu na ninyi, wana wa Rubeni na wana wa Gadi, yaani, Yordani. Hamna fungu lolote katika Yehova.”+ Na wana wenu watawafanya wana wetu waache kumwogopa Yehova.’+

26 “Basi tukasema, ‘Tafadhali, na tuchukue hatua kwa ajili yetu wenyewe, kwa kuijenga madhabahu, si kwa ajili ya toleo la kuteketezwa wala kwa ajili ya dhabihu, 27 bali iwe ushahidi kati yetu+ na ninyi na vizazi vyetu baada yetu kwamba tutafanya utumishi wa Yehova mbele zake kwa matoleo yetu ya kuteketezwa na dhabihu zetu za ushirika,+ ili wana wenu wasiwaambie hivi wana wetu siku fulani wakati ujao: “Ninyi hamna fungu lolote katika Yehova.”’ 28 Basi tukasema, ‘Na itatukia kwamba wakituambia hivyo sisi, na kuwaambia hivyo vizazi vyetu siku fulani wakati ujao, sisi nasi tutasema: “Oneni mfano wa madhabahu ya Yehova ambao baba zetu waliufanya, si kwa ajili ya matoleo ya kuteketezwa wala kwa ajili ya dhabihu, bali huu ni ushahidi kati yetu na ninyi.”’ 29 Ni jambo lisiloweza kuwaziwa, kwa upande wetu, kwamba tumwasi Yehova kwa kupenda kwetu wenyewe na tugeuke nyuma leo tusimfuate Yehova+ kwa kujenga madhabahu kwa ajili ya matoleo ya kuteketezwa, toleo la nafaka na dhabihu zaidi ya ile madhabahu ya Yehova Mungu wetu ambayo iko mbele ya maskani yake!”+

30 Sasa Finehasi+ kuhani na wakuu wa kusanyiko+ na vichwa vya maelfu ya Israeli waliokuwa pamoja naye waliposikia maneno hayo ambayo walisema wana wa Rubeni na wana wa Gadi na wana wa Manase, ikawa vema machoni pao. 31 Basi Finehasi mwana wa Eleazari kuhani akawaambia wana wa Rubeni na wana wa Gadi na wana wa Manase: “Leo tunajua kwamba Yehova yupo katikati yetu,+ kwa kuwa ninyi hamkufanya tendo hili la kukosa uaminifu juu ya Yehova. Basi sasa mmewakomboa wana wa Israeli kutoka katika mkono wa Yehova.”+

32 Ndipo Finehasi mwana wa Eleazari kuhani na wale wakuu wakarudi+ kutoka kwa wana wa Rubeni na wana wa Gadi katika nchi ya Gileadi, wakaenda katika nchi ya Kanaani kwa wale wana wengine wa Israeli, wakawaletea habari.+ 33 Nayo habari hiyo ikawa njema machoni pa wana wa Israeli; nao wana wa Israeli wakambariki Mungu,+ wala hawakuongea kuhusu kwenda katika utumishi wa kijeshi juu yao ili kuiharibu nchi ambayo wana wa Rubeni na wana wa Gadi walikuwa wakikaa.

34 Nao wana wa Rubeni na wana wa Gadi wakaipa madhabahu hiyo jina, kwa sababu “hiyo ni ushahidi kati yetu kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli.”+

23 Na ikawa kwamba baada ya siku nyingi Yehova alipokuwa amekwisha kuwapa Israeli pumziko+ kutoka kwa adui zao wote kuzunguka pande zote, wakati Yoshua alipokuwa mzee na mwenye siku nyingi,+ 2 ndipo Yoshua akaita Israeli wote,+ wanaume wao wazee na wakuu wao na waamuzi wao na maofisa wao,+ naye akawaambia: “Mimi nimekuwa mzee, siku zangu zimekuwa nyingi. 3 Lakini ninyi, mmeona mambo yote ambayo Yehova Mungu wenu aliyatendea mataifa haya yote kwa ajili yenu,+ kwa maana Yehova Mungu wenu ndiye aliyekuwa akiwapigania ninyi.+ 4 Oneni, niliwagawia kwa kura+ mataifa haya yanayobaki yawe urithi kwa ajili ya makabila yenu, na mataifa yote ambayo nilikatilia mbali,+ kuanzia Yordani mpaka Bahari Kuu upande wa magharibi.+ 5 Na Yehova Mungu wenu ndiye aliyeendelea kuwasukuma mbali kutoka mbele yenu,+ naye akawanyang’anya miliki yao kwa ajili yenu, nanyi mkaimiliki nchi yao, kama vile Yehova Mungu wenu alivyokuwa amewaahidi ninyi.+

6 “Nanyi muwe hodari+ sana ili mshike na kufanya yote ambayo yameandikwa katika kitabu+ cha sheria ya Musa kwa kutogeuka kamwe kutoka ndani yake kwenda kuume wala kushoto,+ 7 kwa kutoingia kamwe kati ya mataifa haya,+ yaani, haya yanayobaki na ninyi. Nanyi msitaje majina ya miungu yao+ wala kuapa kwa hiyo,+ msiitumikie wala kuiinamia.+ 8 Bali Yehova Mungu wenu ndiye mnayepaswa kushikamana naye,+ kama vile ambavyo mmefanya mpaka leo hii. 9 Na Yehova atayafukuza mataifa makubwa na yenye nguvu kutoka mbele yenu.+ (Lakini kwenu ninyi, hakuna hata mwanadamu mmoja ambaye amesimama mbele yenu mpaka leo hii.)+ 10 Mtu mmoja tu kati yenu atafukuza elfu,+ kwa maana Yehova Mungu wenu ndiye anayewapigania ninyi,+ kama vile ambavyo amewaahidi ninyi.+ 11 Nanyi lindeni nafsi zenu+ kwa kumpenda Yehova Mungu wenu.+

12 “Lakini mkirudi nyuma kwa vyovyote+ na kushikamana na mabaki ya mataifa haya,+ yaani, haya yanayobaki na ninyi, na kufanya nao mapatano ya ndoa+ na kuingia katikati yao, nao wakiingia katikati yenu, 13 mnapaswa kujua hakika kwamba Yehova Mungu wenu hataendelea kuyanyang’anya mataifa haya miliki yao kwa ajili yenu;+ nayo yatakuwa kwenu kama mtego na mnaso na kama kiboko mbavuni mwenu+ na kama miiba machoni penu mpaka mtakapoangamia na kutoka katika nchi hii nzuri ambayo Yehova Mungu wenu amewapa ninyi.+

14 “Basi sasa, tazameni! leo mimi ninaenda katika njia ya dunia yote,+ nanyi mnajua vema kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi zenu zote kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya hayo.+ 15 Na itatukia kwamba, kama vile neno lote jema ambalo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi limewafikia ninyi,+ vivyo hivyo Yehova ataleta juu yenu neno lote ovu mpaka atakapokuwa amewaangamiza ninyi kutoka katika nchi hii nzuri ambayo Yehova Mungu wenu amewapa ninyi,+ 16 kwa sababu ya kuvunja agano la Yehova Mungu wenu ambalo aliwaamuru ninyi, na kwa sababu mmeenda na kuitumikia miungu mingine na kuiinamia.+ Na hasira ya Yehova hakika itawaka juu yenu,+ nanyi hakika mtaangamia upesi kutoka katika hii nchi nzuri ambayo amewapa.”+

24 Na ndipo Yoshua akakusanya pamoja makabila yote ya Israeli katika Shekemu,+ akawaita wanaume wazee wote wa Israeli+ na vichwa vyao na waamuzi wao na maofisa wao, nao wakasimama mbele za Mungu wa kweli.+ 2 Naye Yoshua akawaambia watu wote: “Yehova Mungu wa Israeli amesema hivi, ‘Mababu+ zenu walikaa ng’ambo ile nyingine ya Mto+ zamani za kale, Tera baba ya Abrahamu na baba ya Nahori,+ nao walikuwa wakiitumikia miungu mingine.

3 “‘Baada ya muda nikamchukua Abrahamu+ babu yenu kutoka ng’ambo ile nyingine ya Mto,+ nikamtembeza katika nchi yote ya Kanaani na kuufanya uzao wake kuwa mwingi.+ Basi nikampa Isaka.+ 4 Ndipo Isaka nikampa Yakobo na Esau.+ Baadaye Esau nikampa Mlima Seiri ili aumiliki;+ na Yakobo na wanawe wakashuka Misri.+ 5 Baadaye nikamtuma Musa na Haruni,+ nami nikapiga Misri kwa yale niliyofanya katikati yake;+ kisha nikawatoa ninyi.+ 6 Nilipokuwa nikiwatoa baba zenu kutoka Misri+ nanyi mkaja kwenye ile bahari, ndipo Wamisri walipowafuatilia+ baba zenu wakiwa na magari ya vita na wapanda-farasi mpaka kwenye Bahari Nyekundu. 7 Nao wakaanza kumlilia Yehova.+ Basi akaweka giza kati yenu na Wamisri,+ naye akaleta bahari juu yao na kuwafunika,+ na macho yenu yakaona mambo niliyoyafanya huko Misri;+ nanyi mkaanza kukaa katika nyika siku nyingi.+

8 “‘Mwishowe nikawaleta ninyi katika nchi ya Waamori waliokuwa wakikaa ng’ambo ile nyingine ya Yordani, nao wakaanza kupigana nanyi.+ Ndipo nikawatia mkononi mwenu ili kuimiliki nchi yao, nami nikawaangamiza kutoka mbele yenu.+ 9 Kisha Balaki mwana wa Sipori,+ mfalme wa Moabu, akasimama na kupigana na Israeli.+ Basi akatuma ujumbe na kumwita Balaamu mwana wa Beori ili awalaani ninyi.+ 10 Nami sikutaka kumsikiliza Balaamu.+ Basi akawabariki ninyi tena na tena.+ Hivyo nikawakomboa kutoka mkononi mwake.+

11 “‘Kisha mkavuka Yordani,+ mkaja Yeriko.+ Nao wenye mashamba wa Yeriko, Waamori na Waperizi na Wakanaani na Wahiti na Wagirgashi, na Wahivi na Wayebusi wakaanza kupigana nanyi; lakini nikawatia mkononi mwenu.+ 12 Basi nikapeleka hisia ya kuvunjika moyo mbele yenu, nayo mwishowe ikawafukuza mbele yenu+—wafalme wawili wa Waamori—haikuwa kwa upanga wenu wala kwa upinde wenu.+ 13 Hivyo nikawapa ninyi nchi ambayo hamkuifanyia kazi ya taabu na majiji ambayo hamkuyajenga,+ nanyi mkakaa ndani yake. Mashamba ya mizabibu na ya mizeituni ambayo hamkupanda ndiyo mnayokula.’+

14 “Na sasa mwogopeni Yehova+ na kumtumikia kwa njia isiyo na kosa na katika kweli,+ nanyi ondoeni miungu ambayo mababu zenu waliitumikia ng’ambo ile nyingine ya Mto na katika Misri,+ mkamtumikie Yehova. 15 Sasa ikiwa mnaona ni vibaya machoni penu kumtumikia Yehova, jichagulieni leo yule mtakayemtumikia,+ kama ni miungu ambayo waliitumikia+ mababu zenu waliokuwa ng’ambo ile nyingine ya Mto au kama ni miungu ya Waamori ambao mnakaa katika nchi yao.+ Lakini mimi na nyumba yangu, tutamtumikia Yehova.”+

16 Ndipo watu wakajibu na kusema: “Ni jambo lisilowaziwa, kwa upande wetu, kumwacha Yehova ili kuitumikia miungu mingine. 17 Kwa maana Yehova Mungu wetu ndiye aliyetuleta sisi na mababu zetu kutoka katika nchi ya Misri,+ kutoka katika nyumba ya watumwa,+ na ambaye alifanya ishara hizi kubwa mbele ya macho yetu,+ akaendelea kutulinda katika njia yote ambayo tulitembea na kati ya watu wote ambao tulipita katikati yao.+ 18 Na Yehova akafukuza vikundi vyote vya watu mbele yetu,+ ndiyo, Waamori, waliokaa mbele yetu katika nchi. Na kwa habari yetu pia, sisi tutamtumikia Yehova, kwa maana yeye ndiye Mungu wetu.”+

19 Ndipo Yoshua akawaambia watu: “Ninyi hamwezi kumtumikia Yehova, kwa maana yeye ni Mungu mtakatifu;+ yeye ni Mungu anayetaka watu wajitoe kikamili.+ Hatasamehe maasi yenu wala dhambi zenu.+ 20 Mkimwacha Yehova+ na kuitumikia miungu ya kigeni,+ yeye hakika atageuka na kuwatendea ninyi madhara na kuwaangamiza baada ya kuwatendea mema.”+

21 Nao watu wakamwambia Yoshua: “Hapana, lakini tutamtumikia Yehova!”+ 22 Ndipo Yoshua akawaambia watu: “Ninyi ni mashahidi dhidi yenu wenyewe+ kwamba mmemchagua Yehova kwa kupenda kwenu wenyewe, ili kumtumikia yeye.”+ Na kwa neno hilo wakajibu: “Sisi ni mashahidi.”

23 “Na sasa ondoeni miungu ya kigeni iliyo katikati yenu,+ mwelekeze mioyo yenu kwa Yehova Mungu wa Israeli.” 24 Ndipo watu hao wakamwambia Yoshua: “Yehova, Mungu wetu, ndiye tutakayemtumikia, na sauti yake ndiyo tutakayoisikiliza!”+

25 Na Yoshua akafanya agano na wale watu siku hiyo na kuwawekea sharti na uamuzi wa hukumu+ katika Shekemu. 26 Ndipo Yoshua akaandika maneno hayo katika kitabu cha sheria ya Mungu,+ akachukua jiwe kubwa,+ akalisimamisha hapo chini ya ule mti mkubwa+ sana ulio kando ya patakatifu pa Yehova.

27 Naye Yoshua akawaambia watu wote: “Tazameni! Jiwe hili litakuwa ushahidi dhidi yetu,+ kwa sababu limesikia maneno yote ya Yehova ambayo amesema nasi, nalo litakuwa ushahidi dhidi yenu, ili msije mkamkana Mungu wenu.” 28 Basi Yoshua akawaacha watu waende zao, kila mmoja kwenye urithi wake.+

29 Na ikawa baada ya mambo hayo, Yoshua mwana wa Nuni mtumishi wa Yehova akafa, akiwa na umri wa miaka mia moja na kumi.+ 30 Basi wakamzika ndani ya eneo la urithi wake katika Timnath-sera,+ lililo katika eneo lenye milima la Efraimu, upande wa kaskazini wa Mlima Gaashi. 31 Na Israeli wakaendelea kumtumikia Yehova siku zote za Yoshua na siku zote za wale wanaume wazee walioendelea kuishi baada ya Yoshua,+ waliokuwa wamejua kazi yote ya Yehova ambayo alifanya kwa ajili ya Israeli.+

32 Na kuhusu ile mifupa ya Yosefu,+ ambayo wana wa Israeli walikuwa wameileta kutoka Misri, waliizika katika Shekemu ndani ya sehemu ya shamba ambalo Yakobo alinunua kutoka kwa wana wa Hamori,+ baba ya Shekemu, kwa vipande mia moja vya pesa;+ nalo likawa urithi wa wana wa Yosefu.+

33 Eleazari mwana wa Haruni akafa pia.+ Basi wakamzika katika Kilima cha Finehasi mwana wake,+ ambacho alikuwa amempa katika eneo lenye milima la Efraimu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki