Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • bi12 Mwanzo 1:1-50:26
  • Mwanzo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mwanzo
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Mwanzo

Mwanzo

1 Hapo mwanzo+ Mungu+ aliumba+ mbingu na dunia.+

2 Dunia ilikuwa bila umbo, na ukiwa, na giza lilikuwa juu ya uso wa kilindi cha maji;+ na nguvu za utendaji za Mungu zilikuwa zikienda huku na huku+ juu ya uso wa maji.+

3 Mungu akasema:+ “Kuwe na nuru.” Kukawa na nuru.+ 4 Kisha Mungu akaona ya kuwa nuru ilikuwa nzuri. Mungu akatenganisha nuru na giza.+ 5 Mungu akaanza kuiita nuru Mchana,+ lakini giza akaliita Usiku.+ Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya kwanza.

6 Mungu akaendelea kusema: “Kuwe na anga+ kati ya hayo maji na mtengano uwepo kati ya maji na maji.”+ 7 Ndipo Mungu akalifanya anga na kutenganisha maji yaliyo chini ya anga na maji yaliyo juu ya anga.+ Ikawa hivyo. 8 Mungu akaanza kuliita anga, Mbingu.+ Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya pili.

9 Mungu akaendelea kusema: “Maji yaliyo chini ya mbingu na yakusanyike mahali pamoja, nayo nchi kavu ionekane.”+ Ikawa hivyo. 10 Na Mungu akaanza kuiita hiyo nchi kavu Dunia,+ lakini mkusanyiko wa maji akauita Bahari.+ Kisha Mungu akaona ya kuwa ilikuwa vyema.+ 11 Mungu akaendelea kusema: “Dunia na itoe majani, mimea inayozaa mbegu,+ miti ya matunda inayozaa matunda kulingana na aina zake,+ ambayo mbegu yake imo ndani yake,+ juu ya nchi.” Ikawa hivyo. 12 Nayo dunia ikaanza kutokeza majani, mimea inayozaa mbegu kulingana na aina yake+ na miti inayozaa matunda, ambayo mbegu yake imo ndani yake kulingana na aina yake.+ Kisha Mungu akaona ya kuwa ilikuwa vyema. 13 Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya tatu.

14 Mungu akaendelea kusema: “Kuwe na mianga katika anga la mbingu ili kutenganisha mchana na usiku;+ nayo iwe ishara na kwa ajili ya majira na kwa ajili ya siku na miaka.+ 15 Nayo iwe mianga katika anga la mbingu ili iangaze dunia.”+ Ikawa hivyo. 16 Na Mungu akaifanya mianga mikubwa miwili. Mwanga mkubwa utawale mchana na mwanga mdogo utawale usiku, na pia nyota.+ 17 Basi Mungu akaiweka katika anga la mbingu ili iangaze dunia,+ 18 na kutawala mchana na usiku na kutenganisha nuru na giza.+ Kisha Mungu akaona ya kuwa ilikuwa vyema.+ 19 Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya nne.

20 Mungu akaendelea kusema: “Maji na yajawe na nafsi hai+ na viumbe vinavyoruka viruke juu ya dunia kwenye uso wa anga la mbingu.”+ 21 Mungu akaanza kuumba wanyama wakubwa mno wa baharini+ na kila nafsi hai inayotembea,+ wakajaa majini kulingana na aina zake, na kila kiumbe kinachoruka chenye mabawa kulingana na aina yake.+ Kisha Mungu akaona ya kuwa ilikuwa vyema. 22 Halafu Mungu akawabariki, akisema: “Zaeni, muwe wengi na kujaza maji yaliyo katika mabonde ya bahari,+ na viumbe vinavyoruka na viwe vingi duniani.” 23 Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya tano.

24 Mungu akaendelea kusema: “Dunia+ na itokeze nafsi zilizo hai kulingana na aina zake, mnyama wa kufugwa+ na mnyama anayetambaa+ na mnyama-mwitu+ wa dunia kulingana na aina yake.” Ikawa hivyo. 25 Mungu akafanya mnyama-mwitu wa dunia kulingana na aina yake na mnyama wa kufugwa kulingana na aina yake na kila mnyama anayetembea wa nchi kulingana na aina yake.+ Mungu akaona ya kuwa ilikuwa vyema.

26 Mungu akaendelea kusema: “Na tufanye+ mtu kwa mfano+ wetu, kwa sura+ yetu, nao watawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na wanyama wa kufugwa na dunia yote na kila mnyama anayetembea juu ya dunia.”+ 27 Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba;+ mwanamume na mwanamke aliwaumba.+ 28 Mungu akawabariki+ na Mungu akawaambia: “Zaeni,+ muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha,+ na mtawale+ samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.”

29 Mungu akaendelea kusema: “Tazama nimewapa mimea yote inayozaa mbegu iliyo juu ya uso wa dunia yote na kila mti ambao una matunda ya mti unaozaa mbegu.+ Na iwe chakula kwenu.+ 30 Na mimea yote ya majani nimetoa iwe chakula+ kwa kila mnyama-mwitu wa dunia na kila kiumbe kinachoruka cha mbinguni na kila kitu kinachotembea juu ya dunia ambacho ndani yake mna uhai ukiwa nafsi.” Ikawa hivyo.

31 Kisha Mungu akaona kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana.+ Ikawa jioni, ikawa asubuhi, siku ya sita.

2 Basi mbingu na dunia na jeshi lake lote zikamalizika.+ 2 Na kufikia siku ya saba Mungu akamaliza kazi yake ambayo alikuwa ameifanya, naye akaanza kupumzika siku ya saba kutokana na kazi yake yote ambayo alikuwa ameifanya.+ 3 Mungu akaibariki siku ya saba na kuifanya takatifu, kwa kuwa katika siku hiyo amekuwa akipumzika kutokana na kazi yake yote ya kuumba ambayo Mungu alikusudia kuifanya.+

4 Hii ndiyo historia ya mbingu na dunia wakati zilipoumbwa, katika siku ambayo Yehova Mungu aliifanya dunia na mbingu.+

5 Basi, mti wa shambani haukuwapo duniani wala mimea ya shambani ilikuwa haijachipuka bado, kwa kuwa Yehova Mungu hakuwa amenyesha mvua+ juu ya dunia wala hapakuwa na mtu wa kuilima nchi. 6 Lakini ukungu+ ulikuwa ukipanda kutoka katika dunia na kuunywesha maji uso wote wa nchi.+

7 Na Yehova Mungu akamfanya mtu kutoka katika mavumbi+ ya nchi+ na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai,+ naye mtu akawa nafsi hai.+ 8 Na Yehova Mungu akapanda bustani katika Edeni,+ kuelekea mashariki, na hapo akamweka mtu ambaye alikuwa amemfanya.+ 9 Hivyo Yehova Mungu akachipusha katika nchi kila mti wenye kutamanika kwa macho ya mtu na ulio mwema kwa ajili ya chakula na pia mti wa uzima+ katikati ya bustani na mti wa ujuzi wa mema na mabaya.+

10 Kulikuwa na mto unaotoka katika Edeni ili kuinywesha bustani maji, na kutoka hapo ukaanza kugawanyika na kuwa vichwa vinne. 11 Jina la ule wa kwanza ni Pishoni; ndio unaozunguka nchi yote ya Havila,+ ambako kuna dhahabu. 12 Nayo dhahabu ya nchi hiyo ni nzuri.+ Pia kuna ulimbo wa bedola+ na jiwe la shohamu.+ 13 Na jina la mto wa pili ni Gihoni; ndio unaozunguka nchi yote ya Kushi. 14 Na jina la mto wa tatu ni Hidekeli;+ ndio unaoelekea upande wa mashariki wa Ashuru.+ Na mto wa nne ni Efrati.+

15 Na Yehova Mungu akamchukua mtu na kumweka katika bustani ya Edeni,+ ailime na kuitunza.+ 16 Pia Yehova Mungu akamwekea mtu amri hii: “Matunda ya kila mti wa bustani unaweza kula mpaka ushibe.+ 17 Lakini kuhusu matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.”+

18 Na Yehova Mungu akaendelea kusema: “Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake. Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.”+ 19 Yehova Mungu alikuwa akifanya kutoka katika udongo kila mnyama wa mwituni na kila kiumbe kinachoruka cha mbinguni, naye akaanza kumletea huyo mtu ili aone atawaitaje kila mmoja wao; na jina ambalo huyo mtu aliita kila nafsi hai,+ kila mmoja, hilo likawa jina lake.+ 20 Basi huyo mtu alikuwa akiita majina wanyama wote wa kufugwa na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila mnyama wa mwituni, lakini kwa ajili ya huyo mwanamume hakupatikana msaidizi wa kuwa kikamilisho chake. 21 Kwa hiyo Yehova Mungu akamletea huyo mwanamume usingizi mzito,+ na alipokuwa akilala, akachukua ubavu wake mmoja na kisha akafunika nyama mahali pake. 22 Na Yehova Mungu akaufanya ubavu ambao alikuwa ameuchukua kutoka kwa mwanamume kuwa mwanamke na kumleta kwa huyo mwanamume.+

23 Ndipo huyo mwanamume akasema:

“Mwishowe huyu ni mfupa wa mifupa yangu

Na nyama ya nyama yangu.+

Huyu ataitwa Mwanamke,

Kwa sababu huyu alitolewa katika mwanamume.”+

24 Hiyo ndiyo sababu mwanamume atamwacha baba yake na mama yake+ naye atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.+ 25 Na wote wawili walikuwa uchi,+ huyo mwanamume na mke wake, lakini hawakuona haya.+

3 Basi nyoka+ alikuwa mwenye kujihadhari+ kuliko wanyama wote wa mwituni ambao Yehova Mungu alikuwa amewafanya.+ Kwa hiyo akaanza kumwambia mwanamke:+ “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?”+ 2 Mwanamke akamjibu na kumwambia nyoka: “Tunaweza kula matunda ya miti ya bustani.+ 3 Lakini kuhusu kula matunda ya mti ulio katikati ya bustani,+ Mungu amesema, ‘Msiyale, wala msiyaguse ili msife.’ ”+ 4 Ndipo nyoka akamwambia mwanamke: “Hakika hamtakufa.+ 5 Kwa maana Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda yake macho yenu yatafunguliwa, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”+

6 Basi mwanamke akaona kwamba mti huo ulikuwa mzuri kwa chakula na kwamba ulikuwa kitu cha kutamanika kwa macho, ndiyo, mti huo ulikuwa wenye kupendeza kuutazama.+ Kwa hiyo akaanza kuchukua kati ya matunda yake akala. Baadaye akampa mume wake pia alipokuwa pamoja naye, naye akaanza kula.+ 7 Ndipo macho yao wote wawili yakafunguliwa nao wakaanza kutambua kwamba walikuwa uchi.+ Kwa hiyo wakashona majani ya mtini ya kujifunika kiunoni.+

8 Baadaye wakasikia sauti ya Yehova Mungu akitembea katika bustani karibu na wakati wenye upepo mtulivu wa siku,+ naye huyo mwanamume na mke wake wakajificha kutoka mbele za uso wa Yehova Mungu katikati ya miti ya bustani.+ 9 Na Yehova Mungu akaendelea kumwita huyo mwanamume na kumuuliza: “Uko wapi?”+ 10 Mwishowe akasema: “Niliisikia sauti yako katika bustani, lakini niliogopa kwa sababu nilikuwa uchi, na basi nikajificha.”+ 11 Ndipo akasema: “Ni nani alikuambia ya kwamba ulikuwa uchi?+ Je, umekula matunda ya mti ambao nilikuamuru usile matunda yake?”+ 12 Na huyo mwanamume akaendelea kusema: “Mwanamke uliyenipa awe pamoja nami, alinipa tunda kutoka katika ule mti nami nikala.”+ 13 Kwa hiyo Yehova Mungu akamwambia mwanamke: “Ni nini hili ulilofanya?” Mwanamke akajibu: “Yule nyoka—alinidanganya nami nikala.”+

14 Na Yehova Mungu akamwambia nyoka:+ “Kwa sababu umefanya jambo hili, umelaaniwa kati ya wanyama wote wa kufugwa na kati ya wanyama wote wa mwituni. Utakwenda kwa tumbo lako na utakula mavumbi siku zote za maisha yako.+ 15 Nami+ nitaweka uadui+ kati yako+ na yule mwanamke+ na kati ya uzao wako+ na uzao wake.+ Yeye+ atakuponda+ kichwa+ nawe+ utamtia jeraha+ kwenye kisigino.”+

16 Akamwambia mwanamke: “Nitazidisha sana maumivu ya mimba yako;+ kwa uchungu utazaa watoto,+ na tamaa yako itakuwa kwa mume wako, naye atakutawala.”+

17 Naye akamwambia Adamu: “Kwa sababu uliisikiliza sauti ya mke wako ukala matunda ya mti ambao nilikupa amri+ hii kuuhusu, ‘Usile matunda yake,’ udongo umelaaniwa kwa sababu yako.+ Kwa maumivu utakula mazao yake siku zote za maisha yako.+ 18 Nao utakuzalia miiba na mibaruti,+ nawe utakula mimea ya shambani. 19 Kwa jasho la uso wako utakula mkate mpaka utakaporudi katika udongo, kwa kuwa ulitolewa katika huo.+ Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.”+

20 Baada ya hayo Adamu akamwita mke wake jina lake Hawa,+ kwa sababu ndiye angekuja kuwa mama ya kila mtu anayeishi.+ 21 Na Yehova Mungu akawafanyia Adamu na mke wake mavazi marefu ya ngozi, akawavika.+ 22 Na Yehova Mungu akaendelea kusema: “Tazama, huyu mtu amekuwa kama mmoja wetu kwa kujua mema na mabaya,+ na sasa ili asije akanyoosha mkono wake achukue matunda kutoka pia katika mti wa uzima+ na kula na kuishi mpaka wakati usio na kipimo,—” 23 Kwa hiyo Yehova Mungu akamwondoa katika bustani ya Edeni+ ili aulime udongo ambao katika huo alikuwa ametolewa.+ 24 Na basi akamfukuza huyo mtu, akaweka upande wa mashariki wa bustani ya Edeni+ makerubi+ na upanga unaowaka ambao ulikuwa unajizungusha-zungusha ili kuilinda njia ya kwenda kwenye ule mti wa uzima.

4 Basi Adamu akalala na Hawa mke wake naye akapata mimba.+ Baada ya muda akamzaa Kaini+ na kusema: “Nimezaa mwanamume kwa msaada wa Yehova.”+ 2 Baadaye akazaa tena, Abeli+ ndugu yake.

Naye Abeli akawa mchungaji wa kondoo,+ bali Kaini akawa mkulima wa udongo.+ 3 Ikawa kwamba baada ya wakati fulani kwisha Kaini akaleta mazao ya udongo+ yawe toleo kwa Yehova.+ 4 Abeli naye akaleta baadhi ya wazaliwa wa kwanza+ wa kundi lake, pia vipande vyao vyenye mafuta.+ Ingawa Yehova alikuwa akimtazama Abeli na toleo lake kwa kibali,+ 5 hakumtazama Kaini na toleo lake kwa kibali chochote.+ Ndipo Kaini akawaka hasira,+ na uso wake ukaanza kukunjamana. 6 Basi Yehova akamwambia Kaini: “Kwa nini umewaka hasira na kwa nini uso wako umekunjamana? 7 Ukigeuka utende mema, je, hutainuliwa?+ Lakini usipogeuka utende mema, kuna dhambi inayovizia katika mwingilio, nayo inakutamani+ wewe. Je, wewe utaishinda?”+

8 Baada ya hayo Kaini akamwambia Abeli ndugu yake: “Twende shambani.” Basi ikawa kwamba walipokuwa shambani Kaini akamshambulia Abeli ndugu yake, akamuua.+ 9 Baadaye Yehova akamuuliza Kaini: “Yuko wapi Abeli ndugu yako?”+ naye akasema: “Sijui. Kwani mimi ni mlinzi wa ndugu yangu?”+ 10 Kwa hiyo akasema: “Umefanya nini? Sikiliza! Damu ya ndugu yako inanililia kutoka katika udongo.+ 11 Na sasa umelaaniwa kwa kufukuzwa kutoka katika udongo,+ ambao umefungua kinywa chake ili kupokea damu ya ndugu yako kwa mkono wako.+ 12 Utakapoulima udongo, hautakurudishia nguvu zake.+ Utakuwa mwenye kutanga-tanga na mkimbizi duniani.”+ 13 Kwa hiyo Kaini akamwambia Yehova: “Adhabu yangu ya kosa ni kubwa mno, haichukuliki. 14 Tazama unanifukuza leo kutoka usoni pa udongo, nami nitafichwa kutoka usoni pako;+ nami nitakuwa mwenye kutanga-tanga+ na mkimbizi duniani, na itakuwa kwamba yeyote atakayenikuta ataniua.”+ 15 Ndipo Yehova akamwambia: “Kwa sababu hiyo yeyote anayemuua Kaini atalipizwa kisasi mara saba.”+

Hivyo Yehova akaweka ishara kwa ajili ya Kaini ili kwamba yeyote anayemkuta asimpige.+ 16 Ndipo Kaini akaenda zake kutoka usoni pa Yehova+ na kukaa katika nchi ya Ukimbizi upande wa mashariki wa Edeni.

17 Baadaye Kaini akalala na mke wake+ naye akapata mimba, akamzaa Enoko. Kisha akajishughulisha na ujenzi wa jiji, akaliita hilo jiji kwa jina la mwana wake Enoko.+ 18 Baadaye Enoko akazaa mwana anayeitwa Iradi. Na Iradi akamzaa Mehuyaeli, na Mehuyaeli akamzaa Methushaeli, na Methushaeli akamzaa Lameki.

19 Na Lameki akajichukulia wake wawili. Jina la wa kwanza lilikuwa Ada na jina la wa pili lilikuwa Zila. 20 Baada ya muda Ada akamzaa Yabali. Akawa mwanzilishi wa wale wanaokaa katika mahema+ na walio na mifugo.+ 21 Na jina la ndugu yake lilikuwa Yubali. Akawa mwanzilishi wa wote wanaotumia kinubi+ na zumari.+ 22 Zila naye pia akamzaa Tubal-kaini, mfuaji wa kila namna ya vifaa vya shaba na chuma.+ Na dada yake Tubal-kaini alikuwa Naama. 23 Basi Lameki akatunga maneno haya kwa ajili ya wake zake Ada na Zila:

“Sikieni sauti yangu, enyi wake za Lameki;

Tegeni sikio kwa maneno yangu:

Nimemuua mtu kwa kunitia jeraha,

Naam, kijana kwa kunipiga.

24 Ikiwa Kaini atalipizwa kisasi mara 7,+

Basi Lameki ni mara 77.”

25 Naye Adamu akalala na mke wake tena naye akazaa mwana, akamwita jina lake Sethi,+ kwa sababu, kama alivyosema: “Mungu amenichagulia uzao mwingine badala ya Abeli, kwa sababu Kaini alimuua.”+ 26 Na Sethi akazaa mwana pia naye akamwita jina lake Enoshi.+ Wakati huo watu wakaanza kuliitia jina la Yehova.+

5 Hiki ndicho kitabu cha historia ya Adamu. Siku ile Mungu alipomuumba Adamu alimfanya kwa mfano wa Mungu.+ 2 Mwanamume na mwanamke aliwaumba.+ Baada ya hapo akawabariki, akawaita jina lao Mwanadamu+ siku ile walipoumbwa.+

3 Naye Adamu akaishi miaka 130. Ndipo akazaa mwana kwa mfano wake, kwa sura yake. Akamwita jina lake Sethi.+ 4 Siku za Adamu baada ya kumzaa Sethi zikawa miaka 800. Wakati uleule akazaa wana na mabinti.+ 5 Kwa hiyo siku zote ambazo Adamu aliishi zikajumlika kuwa miaka 930, naye akafa.+

6 Naye Sethi akaishi miaka 105. Ndipo akamzaa Enoshi.+ 7 Na baada ya kumzaa Enoshi, Sethi akaishi miaka 807. Wakati uleule akazaa wana na mabinti. 8 Basi siku zote za Sethi zikawa miaka 912, naye akafa.

9 Enoshi akaishi miaka 90. Ndipo akamzaa Kenani.+ 10 Na baada ya kumzaa Kenani, Enoshi akaishi miaka 815. Wakati uleule akazaa wana na mabinti. 11 Basi siku zote za Enoshi zikawa miaka 905, naye akafa.

12 Naye Kenani akaishi miaka 70. Ndipo akamzaa Mahalaleli.+ 13 Na baada ya kumzaa Mahalaleli, Kenani akaishi miaka 840. Wakati uleule akazaa wana na mabinti. 14 Basi siku zote za Kenani zikawa miaka 910, naye akafa.

15 Naye Mahalaleli akaishi miaka 65. Ndipo akamzaa Yaredi.+ 16 Na baada ya kumzaa Yaredi, Mahalaleli akaishi miaka 830. Wakati uleule akazaa wana na mabinti. 17 Basi siku zote za Mahalaleli zikawa miaka 895, naye akafa.

18 Na Yaredi akaishi miaka 162. Ndipo akamzaa Enoko.+ 19 Na baada ya kumzaa Enoko, Yaredi akaishi miaka 800. Wakati uleule akazaa wana na mabinti. 20 Basi siku zote za Yaredi zikawa miaka 962, naye akafa.

21 Na Enoko akaishi miaka 65. Ndipo akamzaa Methusela.+ 22 Na baada ya kumzaa Methusela, Enoko akaendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli miaka 300. Wakati uleule akazaa wana na mabinti. 23 Basi siku zote za Enoko zikawa miaka 365. 24 Naye Enoko akaendelea kutembea+ pamoja na Mungu wa kweli.+ Kisha hakuwapo tena, kwa maana Mungu alimchukua.+

25 Naye Methusela akaishi miaka 187. Ndipo akamzaa Lameki.+ 26 Na baada ya kumzaa Lameki, Methusela akaishi miaka 782. Wakati uleule akazaa wana na mabinti. 27 Basi siku zote za Methusela zikawa miaka 969, naye akafa.

28 Naye Lameki akaishi miaka 182. Ndipo akamzaa mwana. 29 Naye akamwita jina lake Noa,+ akisema: “Huyu atatuletea faraja katika kazi yetu na katika maumivu ya mikono yetu yanayoletwa na udongo ambao Yehova amelaani.”+ 30 Na baada ya kumzaa Noa, Lameki akaishi miaka 595. Wakati uleule akazaa wana na mabinti. 31 Basi siku zote za Lameki zikawa miaka 777, naye akafa.

32 Naye Noa akafikia umri wa miaka 500. Baada ya hapo Noa akazaa Shemu,+ Hamu+ na Yafethi.+

6 Sasa ikawa kwamba hesabu ya wanadamu ilipoanza kuongezeka usoni pa nchi nao wakazaa mabinti,+ 2 ndipo wana wa Mungu wa kweli+ wakaanza kuwaona+ mabinti wa wanadamu, kwamba ni wenye sura ya kupendeza; nao wakajichukulia wake, yaani, wote waliowachagua. 3 Baada ya hapo Yehova akasema: “Roho yangu+ haitavumiliana sikuzote+ na mwanadamu kwa kuwa yeye pia ni mwili.+ Kwa hiyo siku zake zitakuwa miaka 120.”+

4 Wanefili walikuwa duniani siku hizo, na pia baada ya hapo, wakati wana wa Mungu wa kweli walipoendelea kulala na binti za wanadamu nao wakawazalia wana, hao ndio waliokuwa watu wenye nguvu wa kale, wanaume wenye sifa.

5 Basi Yehova akaona kuwa ubaya wa mwanadamu ulikuwa mwingi duniani na kila mwelekeo+ wa fikira za moyo wake ulikuwa mbaya tu wakati wote.+ 6 Yehova akajuta+ kwamba amewafanya wanadamu duniani, naye akaumia moyoni+ mwake. 7 Kwa hiyo Yehova akasema: “Nitawafutilia mbali kutoka usoni pa nchi wanadamu ambao nimeumba,+ mwanadamu na mnyama wa kufugwa, na mnyama anayetembea na kiumbe kinachoruka cha mbinguni,+ kwa sababu ninajuta kwamba nimevifanya.”+ 8 Lakini Noa akapata kibali machoni pa Yehova.

9 Hii ndiyo historia ya Noa.

Noa alikuwa mtu mwadilifu.+ Alionekana kuwa mtu asiye na kosa kati ya watu wa siku zake. Noa alitembea pamoja na Mungu wa kweli.+ 10 Baada ya muda Noa akazaa wana watatu, Shemu, Hamu na Yafethi.+ 11 Na dunia ikaharibika machoni pa Mungu wa kweli,+ dunia ikajaa jeuri.+ 12 Basi Mungu akaiona dunia na, tazama! ilikuwa imeharibika,+ kwa sababu kila mwenye mwili alikuwa amejiharibia njia yake duniani.+

13 Baada ya hapo Mungu akamwambia Noa: “Mwisho wa wote wenye mwili umekuja mbele zangu,+ kwa maana dunia imejaa jeuri kwa sababu yao; na tazama mimi ninawaharibu pamoja na dunia.+ 14 Jifanyie safina ya mti wenye utomvu.+ Nawe utafanya vyumba katika safina hiyo, nawe uifunike kwa lami+ ndani na nje. 15 Na hivi ndivyo utakavyoifanya: urefu wa safina utakuwa mikono+ 300, upana wake mikono 50, na kimo chake kitakuwa mikono 30. 16 Utaifanyia safina tsohari [paa; au, dirisha], nawe utaikamilisha kiasi cha mkono mmoja kwenda juu, na mwingilio wa safina utauweka katika ubavu+ wake; utaifanya ikiwa na ghorofa ya chini, ghorofa ya pili na ghorofa ya tatu.

17 “Tazama, mimi ninaleta gharika+ ya maji duniani ili kuharibu kutoka chini ya mbingu wote wenye mwili walio na nguvu za uhai ndani yao.+ Kila kitu kilicho duniani kitakata pumzi.+ 18 Nami ninafanya agano langu pamoja nawe; nawe uingie ndani ya safina, wewe na wana wako na mke wako na wake za wana wako pamoja nawe.+ 19 Na kati ya kila kiumbe hai cha mwili wa aina yote,+ wawili wa kila aina utawaleta ndani ya safina ili kuwahifadhi hai pamoja nawe.+ Watakuwa dume na jike. 20 Kati ya viumbe vinavyoruka kulingana na aina zake na wanyama wa kufugwa kulingana na aina zake,+ kati ya wanyama wote wanaotembea katika nchi kulingana na aina zake, wawili wa kila aina wataingia humo pamoja nawe ili kuwahifadhi hai.+ 21 Wewe nawe, jichukulie kila aina ya chakula kinacholiwa;+ nawe ujikusanyie, kiwe chakula kwa ajili yako na kwa ajili yao.”+

22 Naye Noa akafanya kulingana na yote ambayo Mungu alikuwa amemwamuru. Alifanya vivyo hivyo.+

7 Kisha Yehova akamwambia Noa: “Ingia ndani ya safina, wewe pamoja na nyumba yako yote,+ kwa maana nimekuona wewe kuwa mwadilifu mbele zangu kati ya kizazi hiki.+ 2 Kati ya kila mnyama aliye safi ujichukulie saba saba, dume na jike lake;+ na kati ya kila mnyama asiye safi wawili tu, dume na jike lake; 3 pia kati ya viumbe vinavyoruka vya mbinguni saba saba, dume na jike,+ ili kuhifadhi hai uzao juu ya uso wa dunia+ yote. 4 Kwa maana baada ya siku 7 nitanyesha mvua+ duniani siku 40 mchana na usiku;+ nami nitafutilia mbali kutoka uso wa nchi kila kitu kilichoko ambacho nimekifanya.”+ 5 Basi Noa akafanya kulingana na yote ambayo Yehova alikuwa amemwamuru.

6 Naye Noa alikuwa na umri wa miaka mia sita wakati gharika ya maji ilipokuja duniani.+ 7 Basi Noa akaingia ndani ya safina, yeye na wanawe na mke wake na wake za wanawe pamoja naye, kabla ya maji ya gharika.+ 8 Kati ya kila mnyama aliye safi na kati ya kila mnyama ambaye si safi na kati ya viumbe vinavyoruka na kila kitu kinachotembea juu ya nchi,+ 9 wakaingia wawili wawili kwa Noa ndani ya safina, dume na jike, kama vile Mungu alivyokuwa amemwamuru Noa. 10 Ikawa kwamba siku saba baadaye maji ya gharika yakaja juu ya dunia.

11 Katika mwaka wa mia sita wa maisha ya Noa, mwezi wa pili, siku ya kumi na saba ya mwezi, katika siku hiyo chemchemi zote za kilindi kikubwa cha maji zilitobolewa na malango ya mbinguni yakafunguliwa.+ 12 Na hiyo mvua kubwa juu ya dunia ikaendelea kwa siku 40,+ mchana na usiku. 13 Siku hiyohiyo Noa akaingia ndani ya safina, yeye na Shemu na Hamu na Yafethi, wana wa Noa,+ na mke wa Noa na wake watatu wa wanawe pamoja naye;+ 14 wao na kila mnyama-mwitu kulingana na aina yake,+ na kila mnyama wa kufugwa kulingana na aina yake, na kila mnyama anayetembea atembeaye juu ya dunia kulingana na aina yake,+ na kila kiumbe kinachoruka kulingana na aina yake,+ kila ndege, kila kiumbe chenye mabawa.+ 15 Nao wakazidi kumwendea Noa ndani ya safina, wawili wawili, kati ya kila namna ya mwili ambamo ndani yake nguvu za uhai zilikuwa zikitenda.+ 16 Na wale waliokuwa wakiingia, dume na jike wa kila namna ya mwili, wakaingia, kama vile Mungu alivyokuwa amemwamuru. Kisha Yehova akafunga mlango nyuma yake.+

17 Na hiyo gharika ikaendelea siku 40 juu ya dunia, na maji yakazidi kuongezeka na kuanza kuiinua safina nayo ikawa inaelea juu ya dunia. 18 Maji yakazidi mno na kuendelea kuongezeka sana juu ya dunia, lakini safina iliendelea kuelea juu ya uso wa maji.+ 19 Maji yakazidi mno duniani hivi kwamba milima yote mirefu ambayo ilikuwa chini ya mbingu zote ikafunikwa.+ 20 Maji yakaizidi mno milima hiyo kufikia kiasi cha mikono kumi na mitano, kisha ikafunikwa.+

21 Basi kila chenye mwili kilichokuwa kikitembea juu ya dunia kikakata pumzi,+ kati ya viumbe vinavyoruka na kati ya wanyama wa kufugwa na kati ya wanyama-mwitu na kati ya viumbe vyote vilivyokuwa vinazaana kwa wingi juu ya dunia, na wanadamu wote.+ 22 Kila kitu ambacho ndani yake pumzi ya nguvu za uhai ilikuwa ikitenda katika mianzi ya pua yake, yaani, vyote ambavyo vilikuwa katika nchi kavu, vikafa.+ 23 Basi akafutilia mbali kila kitu kilicho hai ambacho kilikuwa juu ya uso wa nchi, mwanadamu na mnyama, na mnyama anayetembea na kiumbe kinachoruka cha mbinguni, navyo vikafutiliwa mbali duniani;+ na Noa peke yake na wale waliokuwa pamoja naye ndani ya safina wakaendelea kuwa hai.+ 24 Na maji yakaendelea kuizidi mno dunia kwa siku 150.

8 Kisha Mungu akamkumbuka+ Noa na kila mnyama-mwitu na kila mnyama wa kufugwa ambaye alikuwa pamoja naye ndani ya safina.+ Mungu akafanya upepo upite juu ya dunia, nayo maji yakaanza kupungua.+ 2 Nazo chemchemi za kilindi cha maji+ na malango+ ya mbinguni zikafungwa, na kwa hiyo mvua kubwa kutoka mbinguni ikazuiliwa. 3 Nayo maji yakaanza kupungua kutoka juu ya dunia, yakapungua hatua kwa hatua; na mwishoni mwa siku 150 maji hayakuwapo.+ 4 Katika mwezi wa saba, siku ya kumi na saba ya mwezi, safina+ ikatua kwenye milima ya Ararati.+ 5 Na maji yakazidi kupungua hatua kwa hatua mpaka mwezi wa kumi. Katika mwezi wa kumi, siku ya kwanza ya mwezi, vilele vya milima vikaonekana.+

6 Basi ikawa kwamba mwishoni mwa siku 40 Noa akafungua dirisha+ la safina ambalo alikuwa amelifanyiza. 7 Baada ya hapo akatuma kunguru,+ naye akaruka-ruka nje, akienda na kurudi, mpaka maji yalipokauka kutoka juu ya dunia.

8 Baadaye akatuma njiwa+ nje ili kuona ikiwa maji yalikuwa yamepungua kutoka katika uso wa nchi. 9 Na yule njiwa hakupata mahali popote pa kupumzisha wayo wa mguu wake. Basi akamrudia katika safina kwa sababu bado maji yalikuwako juu ya uso wa dunia yote.+ Kwa hiyo akaunyoosha mkono wake na kumchukua. Akamwingiza ndani ya safina. 10 Naye akaendelea kungoja siku saba tena, na mara nyingine tena akamtuma yule njiwa nje ya safina. 11 Baadaye yule njiwa akamjia karibu na wakati wa jioni na, tazama! jani bichi la mzeituni+ lilikuwa katika mdomo wake. Basi Noa akajua kwamba maji yalikuwa yamepungua kutoka juu ya dunia.+ 12 Naye akaendelea kungoja siku saba tena. Ndipo akamtuma yule njiwa, lakini hakurudi kwake tena kamwe.+

13 Basi katika mwaka wa mia sita na moja,+ mwezi wa kwanza, siku ya kwanza ya mwezi, ikawa kwamba maji yalikuwa yamepungua kutoka juu ya dunia; Noa akakiondoa kifuniko cha safina akaona, na tazama, uso wa nchi ulikuwa umekauka kabisa.+ 14 Na katika mwezi wa pili, siku ya 27 ya mwezi, dunia ilikuwa imekauka.+

15 Sasa Mungu akasema na Noa, akamwambia: 16 “Toka nje ya safina, wewe na mke wako na wana wako na wake za wana wako pamoja nawe.+ 17 Kila kiumbe hai kilicho pamoja nawe chenye mwili wa kila namna,+ kati ya viumbe vinavyoruka+ na kati ya wanyama+ na kati ya wanyama wote wanaotembea ambao hutembea juu ya dunia,+ toka nao nje, kwa kuwa wanapaswa kujaa duniani, wazaane na kuwa wengi duniani.”+

18 Ndipo Noa akatoka nje, na wanawe+ pia na mke wake na wake za wanawe pamoja naye. 19 Kila kiumbe hai, kila mnyama anayetembea na kila kiumbe kinachoruka, kila kitu kinachotembea juu ya dunia, kulingana na familia zao walitoka nje ya safina.+ 20 Noa akamjengea Yehova madhabahu+ na kuchukua baadhi ya wanyama wote walio safi+ na baadhi ya viumbe vyote vinavyoruka ambavyo ni safi,+ akatoa matoleo ya kuteketezwa juu ya ile madhabahu.+ 21 Na Yehova akaanza kunusa harufu ya kutuliza,+ na kwa hiyo Yehova akasema moyoni mwake:+ “Sitailaani nchi+ tena kamwe kwa sababu ya mwanadamu, kwani mwelekeo+ wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu ujana wake na kuendelea;+ nami sitakipiga tena kamwe kila kitu chenye uhai kama vile nilivyofanya.+ 22 Siku zote ambazo dunia inaendelea kuwapo, kupanda mbegu na kuvuna, baridi na joto, majira ya kiangazi na majira ya baridi kali, mchana na usiku, havitakoma kamwe.”+

9 Naye Mungu akambariki Noa na wanawe, akawaambia: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia.+ 2 Kila kiumbe hai cha dunia na kila kiumbe kinachoruka cha mbinguni kitawahofu na kuwaogopa ninyi, na pia kila kitu kinachotembea juu ya nchi, na samaki wote wa baharini. Vimetiwa mkononi mwenu.+ 3 Kila mnyama anayetembea ambaye yuko hai anaweza kuwa chakula chenu.+ Kama nilivyowapa mimea ya majani, nawapeni hao wote.+ 4 Isipokuwa tu nyama pamoja na nafsi+ yake—damu+ yake—msile.+ 5 Na, tena, damu ya nafsi zenu nitaitaka. Kwa mkono wa kila kiumbe kilicho hai nitaitaka; na kwa mkono wa mwanadamu, kwa mkono wa kila mmoja ambaye ni ndugu yake, nitaitaka nafsi ya mwanadamu.+ 6 Yeyote anayemwaga damu ya mwanadamu, damu yake nayo itamwagwa na mwanadamu,+ kwa maana kwa mfano wa Mungu alimfanya mwanadamu. 7 Nanyi, zaeni na kuwa wengi, mjaze dunia na kuwa wengi ndani yake.”+

8 Tena Mungu akamwambia Noa na wanawe pamoja naye: 9 “Tazama, mimi nafanya agano+ langu pamoja nanyi na pamoja na wazao wenu baada yenu,+ 10 na pamoja na kila nafsi iliyo hai ambayo iko pamoja nanyi, kati ya ndege, kati ya wanyama na kati ya viumbe vyote vilivyo hai vya dunia ambavyo viko pamoja nanyi, kuanzia vyote vinavyotoka katika safina mpaka kila kiumbe kilicho hai cha dunia.+ 11 Ndiyo, ninafanya agano langu pamoja nanyi: Mwili wote hautakatiliwa mbali tena kwa maji ya gharika, wala hakutatokea tena gharika ya kuiharibu dunia.”+

12 Kisha Mungu akasema tena: “Hii ndiyo ishara+ ya agano ambalo ninaweka kati yangu nanyi na kila nafsi iliyo hai ambayo iko pamoja nanyi, kwa vizazi vyote hata wakati usio na kipimo. 13 Ninawapa upinde wangu wa mvua+ katika wingu, nao utakuwa ishara ya agano lililo kati yangu na dunia. 14 Na itakuwa kwamba ninapoleta wingu juu ya dunia, ndipo upinde wa mvua utakapoonekana katika wingu hilo. 15 Nami nitalikumbuka agano langu+ ambalo liko kati yangu nanyi na kila nafsi iliyo hai kati ya wote wenye mwili;+ na maji hayatakuwa gharika tena ili kuuharibu mwili wote.+ 16 Nao upinde wa mvua utatokea katika wingu,+ nami nitauona na kulikumbuka agano la mpaka wakati usio na kipimo+ kati ya Mungu na kila nafsi iliyo hai kati ya mwili wote ulio duniani.”+

17 Naye Mungu akamwambia tena Noa: “Hiyo ndiyo ishara ya agano ambalo naweka kati yangu na wote wenye mwili walio duniani.”+

18 Wana wa Noa+ waliotoka katika safina walikuwa Shemu na Hamu na Yafethi. Baadaye Hamu akamzaa Kanaani.+ 19 Hao watatu walikuwa wana wa Noa, na kutokana nao watu wote wa dunia walienea kotekote.+

20 Sasa Noa akaanza kuwa mkulima,+ akapanda shamba la mizabibu.+ 21 Akanywa divai na kulewa.+ Akajifunua katikati ya hema lake. 22 Baadaye Hamu+ baba ya Kanaani akauona uchi wa baba yake+ naye akaenda kuwaambia ndugu zake wawili waliokuwa nje.+ 23 Ndipo Shemu na Yafethi wakachukua nguo ya kujitanda+ na kuiweka kwenye mabega yao mawili. Wakatembea kinyume-nyume. Wakaufunika uchi wa baba yao, nyuso zao zikiwa zimegeuzwa, nao hawakuuona uchi wa baba yao.+

24 Mwishowe Noa akaamka kutoka katika divai yake akapata kujua jambo ambalo mwana wake mdogo alikuwa amemfanyia. 25 Basi akasema:

“Alaaniwe Kanaani.+

Na awe mtumwa wa hali ya chini kabisa kwa ndugu zake.”+

26 Naye akasema tena:

“Abarikiwe Yehova,+ Mungu wa Shemu,

Kanaani na awe mtumwa wake.+

27 Mungu na ampe Yafethi nafasi ya kutosha,

Akae katika mahema ya Shemu.+

Kanaani na awe mtumwa wake pia.”

28 Na Noa akaendelea kuishi miaka 350 baada ya gharika.+ 29 Basi siku zote za Noa zikawa miaka 950, naye akafa.+

10 Na hii ndiyo historia ya wana wa Noa,+ yaani, Shemu, Hamu na Yafethi.

Sasa wakaanza kuzaa wana baada ya gharika.+ 2 Wana wa Yafethi walikuwa Gomeri+ na Magogu+ na Madai+ na Yavani+ na Tubali+ na Mesheki+ na Tirasi.+

3 Na wana wa Gomeri walikuwa Ashkenazi+ na Rifathi+ na Togarma.+

4 Na wana wa Yavani walikuwa Elisha+ na Tarshishi,+ Kitimu+ na Dodanimu.+

5 Kutokana na hawa, watu wa visiwa vya mataifa wakaenea kotekote katika nchi zao, kila mmoja kulingana na lugha yake, kulingana na familia zao, kulingana na mataifa yao.

6 Na wana wa Hamu walikuwa Kushi+ na Misraimu+ na Putu+ na Kanaani.+

7 Na wana wa Kushi walikuwa Seba+ na Havila na Sabta na Raama+ na Sabteka.

Na wana wa Raama walikuwa Sheba na Dedani.+

8 Na Kushi akamzaa Nimrodi.+ Akawa wa kwanza kuwa mwenye nguvu duniani. 9 Akajionyesha kuwa mwindaji mwenye nguvu kwa kumpinga Yehova. Hiyo ndiyo sababu kuna msemo: “Kama tu Nimrodi, mwindaji mwenye nguvu kwa kumpinga Yehova.”+ 10 Nao mwanzo wa ufalme wake ukawa Babeli+ na Ereki+ na Akadi na Kalne, katika nchi ya Shinari.+ 11 Akatoka katika nchi ile akaingia Ashuru+ na kuanza kujenga Ninawi+ na Rehoboth-Iri na Kala. 12 na Reseni kati ya Ninawi na Kala: hili ndilo lile jiji kubwa.

13 Naye Misraimu+ akamzaa Ludimu+ na Anamimu na Lehabimu na Naftuhimu+ 14 na Pathrusimu+ na Kasluhimu+ (ambao Wafilisti+ walitokana nao) na Kaftorimu.+

15 Naye Kanaani akamzaa Sidoni,+ mzaliwa wake wa kwanza, na Hethi+ 16 na Myebusi+ na Mwamori+ na Mgirgashi 17 na Mhivi+ na Mwarkia na Msini 18 na Mwarvadi+ na Msemari na Mhamathi;+ baadaye familia za Mkanaani zikatawanyika. 19 Basi mpaka wa Mkanaani ukawa kutoka Sidoni mpaka Gerari,+ karibu na Gaza,+ mpaka Sodoma na Gomora+ na Adma+ na Seboiimu,+ karibu na Lasha. 20 Hao ndio waliokuwa wana wa Hamu kulingana na familia zao, kulingana na lugha zao, katika nchi zao, kulingana na mataifa yao.

21 Naye Shemu, babu ya wana wote wa Eberi,+ ndugu ya Yafethi mkubwa kuliko wote, pia alizaa watoto. 22 Wana wa Shemu walikuwa Elamu+ na Asihuru+ na Arpakshadi+ na Ludi na Aramu.

23 Na wana wa Aramu walikuwa Usi na Huli na Getheri na Mashi.+

24 Naye Arpakshadi akamzaa Shela,+ na Shela akamzaa Eberi.

25 Naye Eberi alizaa wana wawili. Jina la mmoja lilikuwa Pelegi,+ kwa sababu katika siku zake dunia ilikuwa imegawanyika;+ na jina la ndugu yake lilikuwa Yoktani.+

26 Naye Yoktani akazaa Almodadi na Shelefu na Hazarmavethi na Yera+ 27 na Hadoramu na Uzali na Dikla+ 28 na Obali na Abimaeli na Sheba+ 29 na Ofiri+ na Havila+ na Yobabu;+ hao wote ndio waliokuwa wana wa Yoktani.

30 Na mahali pao pa kukaa pakaenea kutoka Mesha mpaka Sefari, eneo lenye milima la Mashariki.

31 Hawa ndio waliokuwa wana wa Shemu kulingana na familia zao, kulingana na lugha zao, katika nchi zao, kulingana na mataifa yao.+

32 Hizi ndizo zilizokuwa familia za wana wa Noa kulingana na ukoo wa familia zao, kulingana na mataifa yao, na kutokana nao mataifa yakaenea kotekote duniani baada ya gharika.+

11 Sasa dunia yote iliendelea kuwa na lugha moja na maneno ya namna moja. 2 Mwishowe ikawa kwamba walipokuwa wakisafiri kuelekea mashariki, waligundua nchi tambarare ya bondeni katika nchi ya Shinari,+ nao wakakaa huko. 3 Nao wakaanza kuambiana: “Haya! Na tutengeneze matofali tuyachome.” Basi matofali yakawa mawe yao, lakini lami ikawa saruji yao.+ 4 Ndipo wakasema: “Haya! Na tujijengee jiji na pia mnara na kilele chake kiwe mbinguni,+ na tujifanyie jina maarufu,+ tusije tukatawanyika juu ya uso wote wa dunia.”+

5 Yehova akashuka aone jiji na mnara ambao wanadamu walikuwa wamejenga.+ 6 Halafu Yehova akasema: “Tazama! Wao ni kikundi kimoja cha watu na wote wana lugha moja,+ na hivi ndivyo wanavyoanza kufanya. Basi sasa hakuna chochote wanachowazia akilini mwao kufanya kitakachowashinda kufikia.+ 7 Haya! Na tushuke,+ tuvuruge+ lugha yao huko ili wasiweze kusikilizana lugha.”+ 8 Basi Yehova akawatawanya juu ya uso wote wa dunia kutoka huko,+ nao pole kwa pole wakaacha kulijenga lile jiji.+ 9 Hiyo ndiyo sababu liliitwa jina lake Babeli,+ kwa sababu huko ndiko Yehova alikuwa amevuruga lugha ya dunia yote, na kutoka huko Yehova alikuwa amewatawanya+ juu ya uso wote wa dunia.

10 Hii ndiyo historia ya Shemu.+

Shemu alikuwa na umri wa miaka 100 wakati alipomzaa Arpakshadi+ miaka miwili baada ya gharika. 11 Na baada ya kumzaa Arpakshadi, Shemu akaishi miaka 500. Wakati uleule akazaa wana na mabinti.+

12 Naye Arpakshadi akaishi miaka 35. Ndipo akamzaa Shela.+ 13 Na baada ya kumzaa Shela, Arpakshadi akaishi miaka 403. Wakati uleule akazaa wana na mabinti.

14 Naye Shela akaishi miaka 30. Ndipo akamzaa Eberi.+ 15 Na baada ya kumzaa Eberi, Shela akaishi miaka 403. Wakati uleule akazaa wana na mabinti.

16 Naye Eberi akaishi miaka 34. Ndipo akamzaa Pelegi.+ 17 Na baada ya kumzaa Pelegi, Eberi akaishi miaka 430. Wakati uleule akazaa wana na mabinti.

18 Naye Pelegi akaishi miaka 30. Ndipo akamzaa Reu.+ 19 Na baada ya kumzaa Reu, Pelegi akaishi miaka 209. Wakati uleule akazaa wana na mabinti.

20 Naye Reu akaishi miaka 32. Ndipo akamzaa Serugi.+ 21 Na baada ya kumzaa Serugi, Reu akaishi miaka 207. Wakati uleule akazaa wana na mabinti.

22 Naye Serugi akaishi miaka 30. Ndipo akamzaa Nahori.+ 23 Na baada ya kumzaa Nahori, Serugi akaishi miaka 200. Wakati uleule akazaa wana na mabinti.

24 Naye Nahori akaishi miaka 29. Ndipo akamzaa Tera.+ 25 Na baada ya kumzaa Tera, Nahori akaishi miaka 119. Wakati uleule akazaa wana na mabinti.

26 Naye Tera akaishi miaka 70, kisha akamzaa Abramu,+ Nahori+ na Harani.

27 Na hii ndiyo historia ya Tera.

Tera akamzaa Abramu, Nahori na Harani; naye Harani akamzaa Loti.+ 28 Baadaye Harani akafa akiwa angali na baba yake Tera katika nchi ya kuzaliwa kwake, katika Uru+ la Wakaldayo.+ 29 Nao Abramu na Nahori wakajichukulia wake. Jina la mke wa Abramu lilikuwa Sarai,+ na jina la mke wa Nahori lilikuwa Milka+ binti ya Harani, baba ya Milka na baba ya Iska. 30 Lakini Sarai aliendelea kuwa tasa;+ hakuwa na mtoto.

31 Baada ya hapo Tera akamchukua mwana wake Abramu, na mjukuu wake Loti,+ mwana wa Harani, na binti-mkwe wake Sarai,+ mke wa mwana wake Abramu, nao wakaondoka Uru la Wakaldayo pamoja naye ili kwenda katika nchi ya Kanaani.+ Baadaye wakaja Harani+ na kukaa huko. 32 Na siku za Tera zikawa miaka 205. Ndipo Tera akafa huko Harani.

12 Naye Yehova akamwambia Abramu: “Nenda zako kutoka katika nchi yako na kutoka kwa watu wa jamaa yako na kutoka kwa nyumba ya baba yako mpaka katika nchi ambayo nitakuonyesha;+ 2 nami nitafanya taifa kubwa kutokana nawe, nitakubariki na kulifanya jina lako kuwa kuu; nawe uwe baraka.+ 3 Nami nitawabariki wale wanaokubariki, na yule anayekulaani nitamlaani,+ na familia zote za nchi zitajibariki kupitia kwako.”+

4 Ndipo Abramu akaenda kama vile Yehova alivyokuwa amemwambia, na Loti akaenda pamoja naye. Na Abramu alikuwa na umri wa miaka 75 alipoondoka Harani.+ 5 Basi Abramu akamchukua Sarai mke wake+ na Loti mwana wa ndugu yake+ na mali zote ambazo walikuwa wamekusanya+ na nafsi ambazo walikuwa wamejipatia katika Harani, nao wakaenda nchi ya Kanaani.+ Mwishowe wakafika katika nchi ya Kanaani. 6 Na Abramu akapita katikati ya nchi mpaka eneo la Shekemu,+ karibu na miti mikubwa ya More;+ wakati huo Mkanaani alikuwa katika nchi hiyo. 7 Ndipo Yehova akamtokea Abramu na kusema: “Nitaupa uzao wako+ nchi hii.”+ Baada ya hayo akajenga madhabahu huko kwa ajili ya Yehova, aliyekuwa amemtokea. 8 Baadaye akaondoka huko kwenda katika eneo lenye milima upande wa mashariki wa Betheli.+ Akapiga hema lake, Betheli likiwa upande wa magharibi, na Ai+ upande wa mashariki. Ndipo akamjengea Yehova madhabahu huko+ naye akaanza kuliitia jina la Yehova.+ 9 Baadaye Abramu akavunja kambi, wakati huo akienda kutoka kambi mpaka kambi kuelekea Negebu.+

10 Sasa njaa ikatokea katika nchi, naye Abramu akateremka kuelekea Misri akakae huko akiwa mgeni,+ kwa sababu njaa ilikuwa kali katika nchi.+ 11 Ikawa mara alipokaribia kuingia Misri, akamwambia Sarai mke wake: “Tafadhali, tazama! najua vema kuwa wewe ni mwanamke mwenye sura nzuri.+ 12 Basi itakuwa kwamba Wamisri watakapokuona watasema, ‘Huyu ni mke wake.’ Nao wataniua, lakini wewe watakuhifadhi hai. 13 Tafadhali sema wewe ni dada yangu,+ ndipo iwe vema kwangu kwa sababu yako, na nafsi yangu itaishi kwa ajili yako.”+

14 Basi ikawa kwamba, mara Abramu alipoingia Misri, Wamisri wakapata kumwona mwanamke huyo, kwamba alikuwa mrembo sana. 15 Na wakuu wa Farao pia wakapata kumwona nao wakaanza kumsifu mbele ya Farao, basi mwanamke huyo akapelekwa nyumbani kwa Farao. 16 Naye akamtendea Abramu vema kwa sababu yake, naye akawa na kondoo na ng’ombe na punda na watumishi wa kiume na wajakazi na punda-jike na ngamia.+ 17 Ndipo Yehova akamgusa Farao na nyumba yake kwa mapigo makubwa+ kwa sababu ya Sarai, mke wa Abramu.+ 18 Basi Farao akamwita Abramu na kusema: “Ni nini hili umenitendea? Kwa nini hukuniambia kwamba yeye ni mke wako?+ 19 Kwa nini ulisema, ‘Yeye ni dada yangu,’+ basi nikawa karibu kumchukua awe mke wangu? Basi mke wako ndiye huyu. Mchukue, uende!” 20 Ndipo Farao akawatolea watu amri kumhusu, nao wakamsindikiza yeye na mke wake na vyote alivyokuwa navyo.+

13 Baada ya hayo Abramu akaondoka Misri, yeye na mke wake na vyote alivyokuwa navyo, na Loti pamoja naye, kwenda Negebu.+ 2 Naye Abramu alikuwa na utajiri mwingi wa mifugo na fedha na dhahabu.+ 3 Naye akaenda kambi kwa kambi kutoka Negebu mpaka Betheli, kwenda mahali ambapo hema lake lilikuwa mara ya kwanza kati ya Betheli na Ai,+ 4 penye madhabahu ambayo alikuwa ameifanya hapo mwanzoni;+ naye Abramu akaliitia jina la Yehova hapo.+

5 Sasa Loti pia, aliyekuwa akienda pamoja na Abramu, alikuwa na kondoo na ng’ombe na mahema. 6 Basi nchi haikuwaruhusu wakae wote pamoja, kwa sababu mali zao zilikuwa zimekuwa nyingi nao hawakuweza kukaa pamoja.+ 7 Na ugomvi ukatokea kati ya wachungaji wa mifugo ya Abramu na wachungaji wa mifugo ya Loti; na wakati huo Mkanaani na Mperizi walikuwa wakikaa katika nchi hiyo.+ 8 Ndipo Abramu akamwambia Loti:+ “Tafadhali, usiruhusu ugomvi wowote uendelee kuwa kati yangu na wewe na kati ya wachungaji wangu na wachungaji wako, kwa kuwa sisi ni ndugu.+ 9 Je, nchi yote haiko mbele yako? Tafadhali, jitenge nami. Ukienda kushoto, mimi nitakwenda kuume; lakini ukienda kuume, mimi nitakwenda kushoto.”+ 10 Basi Loti akainua macho yake na kuona Wilaya yote ya Yordani,+ kwamba yote ilikuwa eneo lililokuwa na maji mengi kabla Yehova hajaharibu Sodoma na Gomora, kama bustani ya Yehova,+ kama nchi ya Misri mpaka Soari.+ 11 Ndipo Loti akajichagulia Wilaya yote ya Yordani. Loti akahamisha kambi yake kuelekea mashariki. Basi wakatengana. 12 Abramu alikaa katika nchi ya Kanaani, lakini Loti akakaa kati ya majiji ya Wilaya hiyo.+ Mwishowe akapiga hema karibu na Sodoma. 13 Basi watu wa Sodoma walikuwa wabaya nao walikuwa wakimtendea Yehova dhambi nzito.+

14 Yehova akamwambia Abramu baada ya Loti kujitenga naye: “Tafadhali, inua macho yako utazame kutoka mahali ulipo, upande wa kaskazini na wa kusini na wa mashariki na wa magharibi,+ 15 kwa kuwa nchi yote ambayo unaitazama, nitakupa wewe na uzao wako hata wakati usio na kipimo.+ 16 Nami nitaufanya uzao wako uwe kama chembe za mavumbi ya dunia, ili, ikiwa mwanadamu angeweza kuzihesabu chembe za mavumbi ya dunia, basi uzao wako ungeweza kuhesabiwa.+ 17 Ondoka, zunguka katika nchi kwa marefu na mapana yake, kwa kuwa hiyo nitakupa wewe.”+ 18 Basi Abramu akaendelea kuishi katika mahema. Baadaye akaja na kukaa kati ya miti mikubwa ya Mamre,+ ambayo iko katika Hebroni;+ na huko akamjengea Yehova madhabahu.+

14 Sasa ikawa siku za Amrafeli mfalme wa Shinari,+ Arioko mfalme wa Elasari, Kedorlaoma+ mfalme wa Elamu,+ na Tidali mfalme wa Goiimu,+ 2 kwamba hao wakafanya vita na Bera mfalme wa Sodoma,+ na Birsha mfalme wa Gomora,+ Shinabu mfalme wa Adma,+ na Shemeberi mfalme wa Seboiimu,+ na mfalme wa Bela (yaani, Soari).+ 3 Hao wote wakaenda pamoja kwa kushirikiana+ mpaka katika Nchi Tambarare ya Chini ya Sidimu,+ yaani, Bahari ya Chumvi.+

4 Walikuwa wamemtumikia Kedorlaoma miaka kumi na miwili, lakini mwaka wa kumi na tatu wakaasi. 5 Na mwaka wa kumi na nne Kedorlaoma akaja, na pia wafalme waliokuwa pamoja naye, nao wakashinda Warefaimu katika Ashteroth-karnaimu,+ na Wazuzi katika Hamu, na Waemi+ katika Shave-kiriathaimu, 6 na Wahori+ katika mlima wao wa Seiri,+ mpaka El-parani,+ ulioko nyikani. 7 Ndipo wakageuka na kuja En-mishpati, yaani, Kadeshi,+ wakashinda shamba lote la Waamaleki+ na pia Waamori+ waliokuwa wakikaa katika Hasason-tamari.+

8 Ndipo mfalme wa Sodoma akapiga mwendo, na pia mfalme wa Gomora na mfalme wa Adma na mfalme wa Seboiimu na mfalme wa Bela (yaani, Soari), nao wakajipanga kivita wapigane nao katika Nchi Tambarare ya Chini ya Sidimu,+ 9 wapigane na Kedorlaoma mfalme wa Elamu na Tidali mfalme wa Goiimu na Amrafeli mfalme wa Shinari na Arioko mfalme wa Elasari;+ wafalme wanne wapigane na watano. 10 Basi Nchi Tambarare ya Chini ya Sidimu+ ilikuwa imejaa mashimo ya lami;+ nao wafalme wa Sodoma na Gomora+ wakakimbia na kuanguka ndani yake, na wale waliobaki wakakimbilia eneo lenye milima.+ 11 Ndipo washindi wakachukua mali zote za Sodoma na Gomora na chakula chao chote, wakaenda zao.+ 12 Pia wakamchukua Loti mwana wa ndugu ya Abramu na mali zake, wakaenda zao. Wakati huo alikuwa akikaa Sodoma.+

13 Baada ya hayo mtu aliyekuwa ameponyoka akaja na kumwambia Abramu Mwebrania.+ Wakati huo alikuwa akikaa kati ya miti mikubwa ya Mamre yule Mwamori,+ ndugu ya Eshkoli na ndugu ya Aneri;+ nao walikuwa washirika wa Abramu. 14 Basi Abramu akasikia kwamba ndugu yake amechukuliwa mateka.+ Kwa hiyo akakusanya watu wake waliozoezwa,+ watumwa mia tatu kumi na wanane waliozaliwa nyumbani mwake,+ akawafuatilia mpaka Dani.+ 15 Na wakati wa usiku akagawa vikosi vyake,+ yeye na watumwa wake, kupigana nao, basi akawashinda na kuendelea kuwafuata mpaka Hoba, upande wa kaskazini wa Damasko. 16 Naye akarudisha mali zote,+ naye akamrudisha pia Loti ndugu yake na mali zake zote na pia wanawake na watu.+

17 Ndipo mfalme wa Sodoma akatoka kwenda kumpokea baada ya kurudi kutoka kumshinda Kedorlaoma na wafalme waliokuwa pamoja naye, katika Nchi Tambarare ya Chini ya Shave, yaani, Nchi Tambarare ya Chini ya mfalme.+ 18 Na Melkizedeki+ mfalme wa Salemu+ akaleta mkate na divai,+ naye alikuwa kuhani wa Mungu Aliye Juu Zaidi.+ 19 Ndipo akambariki na kusema:

“Abarikiwe Abramu wa Mungu Aliye Juu Zaidi,+

Yeye aliyezitokeza mbingu na dunia;+

20 Na abarikiwe Mungu Aliye Juu Zaidi,+

Ambaye amewatia wakandamizaji wako mkononi mwako!”+

Kisha Abramu akampa sehemu ya kumi ya kila kitu.+

21 Baada ya hayo mfalme wa Sodoma akamwambia Abramu: “Nipe nafsi hizo,+ lakini ujichukulie mali.” 22 Ndipo Abramu akamwambia mfalme wa Sodoma: “Nainua mkono wangu katika kiapo+ kwa Yehova Mungu Aliye Juu Zaidi, Mtokezaji wa mbingu na dunia, 23 kwamba, wala uzi wala kamba ya kiatu, sitachukua kitu kutoka kwa chochote kilicho chako,+ usije ukasema, ‘Ni mimi niliyemtajirisha Abramu.’ 24 Sitaki chochote!+ Isipokuwa tu kile ambacho vijana wamekula tayari, na fungu la watu walioenda nami, Aneri, Eshkoli na Mamre+—na wachukue fungu lao.”+

15 Baada ya mambo hayo neno la Yehova likamjia Abramu katika maono,+ na kusema: “Usiogope,+ Abramu. Mimi ni ngao kwako.+ Thawabu yako itakuwa kubwa sana.”+ 2 Ndipo Abramu akasema: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, utanipa nini, kwa sababu mimi naenda zangu bila mtoto na yule atakayeirithi nyumba yangu ni Eliezeri,+ mtu wa Damasko?” 3 Kisha Abramu akasema tena: “Tazama! Hukunipa uzao+ wowote, na, tazama! mwana+ wa nyumba yangu anakuwa mrithi wangu.” 4 Lakini, tazama! neno la Yehova likamjia kwa maneno haya: “Mtu huyu hatakuwa mrithi wako, lakini yule atakayetoka katika viuno vyako mwenyewe ndiye atakayekuwa mrithi wako.”+

5 Ndipo akamtoa nje na kusema: “Tafadhali, tazama juu mbinguni uzihesabu nyota, ikiwa unaweza kuzihesabu.”+ Naye akaendelea kumwambia: “Ndivyo utakavyokuwa uzao wako.”+ 6 Naye akawa na imani katika Yehova;+ naye akamhesabia kuwa ni uadilifu.+ 7 Ndipo akaongeza kumwambia: “Mimi ni Yehova, niliyekutoa katika Uru la Wakaldayo ili nikupe nchi hii uirithi.”+ 8 Akajibu akasema: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, nitajuaje kwamba nitairithi?”+ 9 Naye akamwambia: “Nichukulie ndama wa miaka mitatu na mbuzi-jike wa miaka mitatu na kondoo-dume wa miaka mitatu na njiwa-tetere na njiwa mchanga.”+ 10 Basi akawachukua wote hao na kuwakata vipande viwili. Akaweka kila kipande chao ili kilingane na kile kingine, lakini wale ndege hakuwakata vipande.+ 11 Na ndege wawindaji wakaanza kushuka juu ya mizoga hiyo,+ lakini Abramu akawa akiwafukuza.

12 Baada ya muda fulani jua likawa karibu kutua, na usingizi mzito ukamshika Abramu,+ na, tazama! giza kubwa la kuogopesha likaanza kumwangukia. 13 Naye akaanza kumwambia Abramu: “Ujue hakika kwamba uzao wako utakuwa mkaaji mgeni katika nchi isiyokuwa yao,+ nao watawatumikia watu wale, nao watawatesa kwa miaka mia nne.+ 14 Lakini taifa watakalolitumikia mimi ninalihukumu,+ na baada ya hapo wataondoka na mali nyingi.+ 15 Lakini wewe, utaenda kwa mababu zako kwa amani; utazikwa katika uzee mwema.+ 16 Lakini katika kizazi cha nne watarudi hapa,+ kwa sababu kosa la Waamori halijawa kamili bado.”+

17 Basi jua lilikuwa likitua na giza kubwa likaja na, tazama! kulikuwa na tanuru linalotoa moshi na mwenge wenye moto uliokuwa ukipita katikati ya vipande hivyo.+ 18 Siku hiyo Yehova akafanya agano na Abramu,+ akisema: “Nitaupatia uzao wako nchi hii,+ kutoka mto wa Misri mpaka ule mto mkubwa, mto Efrati:+ 19 Wakeni+ na Wakenizi na Wakadmoni 20 na Wahiti+ na Waperizi+ na Warefaimu+ 21 na Waamori na Wakanaani na Wagirgashi na Wayebusi.”+

16 Sasa Sarai, mke wa Abramu, hakuwa amemzalia watoto wowote;+ lakini alikuwa na mjakazi Mmisri na jina lake lilikuwa Hagari.+ 2 Ndipo Sarai akamwambia Abramu: “Tafadhali sasa! Yehova amenifunga nisizae watoto.+ Tafadhali, lala na mjakazi wangu. Labda ninaweza kupata watoto kutokana naye.”+ Basi Abramu akaisikiliza sauti ya Sarai.+ 3 Ndipo Sarai, mke wa Abramu, akamchukua Hagari, mjakazi wake Mmisri, mwishoni mwa miaka kumi ya kukaa kwa Abramu katika nchi ya Kanaani, naye akampa mume wake Abramu kama mke wake.+ 4 Basi akalala na Hagari, naye akapata mimba. Wakati alipojua kwamba ana mimba, ndipo bimkubwa wake akawa mtu wa kudharaulika machoni pake.+

5 Basi Sarai akamwambia Abramu: “Jeuri niliyotendewa na iwe juu yako. Mimi nilimtia mjakazi wangu kifuani pako, naye alipojua kwamba ana mimba, akaanza kunidharau machoni pake. Yehova na ahukumu kati yangu na wewe.”+ 6 Ndipo Abramu akamwambia Sarai:+ “Tazama! Mjakazi wako yuko chini ya mamlaka yako. Mtendee yaliyo mema machoni pako.”+ Basi Sarai akaanza kumfedhehesha hivi kwamba akakimbia kutoka kwake.+

7 Baadaye malaika wa Yehova+ akamkuta kwenye chemchemi ya maji nyikani, kwenye chemchemi iliyo njiani kuelekea Shuri.+ 8 Naye akaanza kusema: “Hagari, mjakazi wa Sarai, umetoka wapi nawe unaenda wapi?” Naye akajibu: “Mimi ninakimbia kutoka kwa Sarai bimkubwa wangu.” 9 Na malaika wa Yehova akaendelea kumwambia: “Rudi kwa bimkubwa wako ujinyenyekeze chini ya mkono wake.”+ 10 Ndipo malaika wa Yehova akamwambia: “Nitauzidisha sana uzao wako,+ hivi kwamba hautahesabiwa kwa sababu ya wingi wake.”+ 11 Tena, malaika wa Yehova akamwambia: “Tazama una mimba, nawe utazaa mwana, nawe utamwita jina lake Ishmaeli;+ kwa kuwa Yehova ameyasikia mateso yako.+ 12 Na yeye atakuwa kama punda-milia. Mkono wake utamwinukia kila mtu, na mkono wa kila mtu utamwinukia yeye;+ naye atakaa mbele ya uso wa ndugu zake wote.”+

13 Ndipo akaanza kuliita jina la Yehova, aliyekuwa akisema naye: “Wewe ni Mungu mwenye kuona,”+ kwa kuwa alisema: “Je, kweli hapa nimemtazama yeye anayeniona?” 14 Hiyo ndiyo sababu kisima hicho kiliitwa Beer-lahai-roi.+ Tazama, kiko kati ya Kadeshi na Beredi. 15 Baadaye Hagari akamzalia Abramu mwana naye Abramu akamwita huyo mwana wake ambaye Hagari alimzalia, jina lake Ishmaeli.+ 16 Naye Abramu alikuwa na umri wa miaka 86 Hagari alipomzalia Ishmaeli.

17 Abramu alipokuwa na umri wa miaka 99, Yehova akamtokea Abramu na kumwambia:+ “Mimi ni Mungu Mweza-Yote.+ Tembea mbele zangu nawe ujionyeshe kuwa huna kosa.+ 2 Nami nitaweka agano langu kati yangu mimi na wewe,+ ili nipate kukuzidisha wewe sana sana.”+

3 Ndipo Abramu akaanguka kifudifudi,+ na Mungu akaendelea kusema naye, na kumwambia: 4 “Kwa habari yangu, tazama! agano langu lipo pamoja na wewe,+ nawe hakika utakuwa baba ya umati wa mataifa.+ 5 Na jina lako halitakuwa Abramu tena, jina lako litakuwa Abrahamu, kwa sababu nitakufanya kuwa baba ya umati wa mataifa. 6 Nami nitakufanya uwe mwenye kuzaa sana sana na kukufanya uwe mataifa, na wafalme watatoka ndani yako.+

7 “Nami nitatimiza agano langu kati yangu mimi na wewe+ na uzao wako baada yako kulingana na vizazi vyao kuwa agano la mpaka wakati usio na kipimo,+ ili kujionyesha mwenyewe kuwa Mungu kwako na kwa uzao wako baada yako.+ 8 Nami nitakupa wewe na uzao wako baada yako ile nchi ya makao yako ya kigeni,+ naam, nchi yote ya Kanaani, ili kuimiliki hata wakati usio na kipimo; nami nitajionyesha mwenyewe kuwa Mungu kwao.”+

9 Na tena Mungu akamwambia Abrahamu: “Kwa habari yako, unapaswa kushika agano langu, wewe na uzao wako baada yako kulingana na vizazi vyao.+ 10 Hili ndilo agano langu ambalo ninyi mtashika, kati yangu na ninyi, hata uzao wako baada yako.+ Kila mwanamume wa kwenu lazima atahiriwe.+ 11 Nanyi mnapaswa kutahiriwa nyama ya magovi yenu, nayo iwe ishara ya agano kati yangu mimi na ninyi.+ 12 Na kila mwanamume wa kwenu wa umri wa siku nane lazima atahiriwe,+ kulingana na vizazi vyenu, yeyote aliyezaliwa ndani ya nyumba na yeyote aliyenunuliwa kwa pesa kutoka kwa mgeni yeyote ambaye si wa uzao wako. 13 Kila mwanamume aliyezaliwa ndani ya nyumba yako na kila mwanamume aliyenunuliwa kwa pesa zako asikose kutahiriwa;+ na agano langu katika miili yenu ninyi wanaume lazima litumike likiwa agano mpaka wakati usio na kipimo.+ 14 Na mwanamume ambaye hajatahiriwa, ambaye hatatahiri nyama ya govi lake, nafsi hiyo lazima ikatiliwe mbali kutoka kwa watu wake.+ Yeye amevunja agano langu.”

15 Naye Mungu akaendelea kumwambia Abrahamu: “Kwa habari ya Sarai mke wako, usimwite jina lake Sarai, kwa sababu Sara ndilo jina lake.+ 16 Nami nitambariki yeye na pia nitakupa mwana kupitia yeye;+ nami nitambariki Sara naye atakuwa mataifa;+ wafalme wa vikundi vya watu watatoka kwake.”+ 17 Ndipo Abrahamu akaanguka kifudifudi, akaanza kucheka na kusema moyoni mwake:+ “Je, mtu wa umri wa miaka 100 atazaa mtoto, na je, Sara, ndiyo, je, mwanamke wa umri wa miaka 90 atazaa?”+

18 Kisha Abrahamu akamwambia Mungu wa kweli: “Laiti Ishmaeli angeishi mbele zako!”+ 19 Basi Mungu akasema: “Sara mke wako kwa kweli atakuzalia mwana, nawe utamwita jina lake Isaka.+ Nami nitafanya agano langu pamoja naye kuwa agano la mpaka wakati usio na kipimo kwa uzao wake baada yake.+ 20 Lakini kuhusu Ishmaeli nimekusikia. Tazama! nitambariki, nimfanye aongezeke na kumzidisha sana sana.+ Hakika atatokeza wakuu kumi na wawili, nami nitamfanya kuwa taifa kubwa.+ 21 Hata hivyo, agano langu nitalifanya pamoja na Isaka,+ ambaye Sara atakuzalia wakati huu uliowekwa mwaka ujao.”+

22 Kwa hayo Mungu akamaliza kusema naye, akaenda zake juu kutoka kwa Abrahamu.+ 23 Ndipo Abrahamu akamchukua Ishmaeli mwana wake na wanaume wote waliozaliwa nyumbani mwake na kila mtu aliyenunuliwa kwa pesa zake, kila mtu wa kiume kati ya wanaume wa nyumba ya Abrahamu, naye akaanza kutahiri nyama ya magovi yao siku hiyo hiyo, kama Mungu alivyokuwa amemwambia.+ 24 Na Abrahamu alikuwa na umri wa miaka 99 alipotahiriwa nyama ya govi lake.+ 25 Na Ishmaeli mwana wake alikuwa na umri wa miaka kumi na mitatu alipotahiriwa nyama ya govi lake.+ 26 Siku hiyo hiyo Abrahamu alitahiriwa, na pia Ishmaeli mwana wake.+ 27 Na wanaume wote wa nyumba yake, yeyote aliyezaliwa nyumbani na yeyote aliyenunuliwa kwa pesa kutoka kwa mgeni, alitahiriwa pamoja naye.+

18 Baadaye Yehova akamtokea+ kati ya miti mikubwa ya Mamre,+ alipokuwa ameketi kwenye mwingilio wa hema karibu na wakati wa joto la mchana.+ 2 Alipoinua macho yake,+ kisha akatazama, kumbe pale, wamesimama wanaume watatu umbali fulani kutoka kwake. Alipowaona akaanza kukimbia awapokee kutoka mwingilio wa hema naye akainama kifudifudi.+ 3 Kisha akasema: “Yehova, ikiwa, sasa, nimepata kibali machoni pako, tafadhali usimpite mtumishi wako.+ 4 Tafadhali, acha maji kidogo yachukuliwe, nanyi mwoshwe miguu yenu.+ Kisha mketi chini ya mti.+ 5 Nanyi acheni nichukue kipande cha mkate, niburudishe mioyo yenu.+ Baadaye, ninyi mnaweza kuendelea mbele, kwa maana hiyo ndiyo sababu mmepitia njia hii kwa mtumishi wenu.” Basi wakasema: “Vema. Unaweza kufanya kama ulivyosema.”

6 Kwa hiyo Abrahamu akafanya haraka kwenda katika hema alimokuwa Sara, akasema: “Fanya haraka! Chukua vipimo vitatu vya sea vya unga laini, ukande donge na kuoka keki za mviringo.”+ 7 Kisha Abrahamu akakimbia kwenye mifugo akachukua ng’ombe-dume mchanga, mzuri na mwororo akampa mtumishi, naye akafanya haraka kumtayarisha.+ 8 Ndipo akachukua siagi na maziwa na yule ng’ombe mchanga ambaye alikuwa amemtayarisha, akaweka mbele yao.+ Kisha yeye akaendelea kusimama kando yao chini ya mti walipokuwa wakila.+

9 Sasa wakamwambia: “Yuko wapi Sara mke wako?”+ Ndipo akasema: “Hapa hemani!”+ 10 Kwa hiyo akaendelea kusema: “Hakika mimi nitarudi kwako mwaka ujao wakati huu, na, tazama! Sara mke wako atapata mwana.”+ Basi Sara alikuwa akisikiliza kwenye mwingilio wa hema, nao ulikuwa nyuma ya mwanamume huyo. 11 Naye Abrahamu na Sara walikuwa wazee, wamesonga katika miaka.+ Sara alikuwa ameacha kuwa na hedhi.+ 12 Kwa hiyo Sara akaanza kucheka ndani yake mwenyewe,+ akisema: “Baada ya mimi kuzeeka, kweli mimi nitapata raha, tena bwana wangu akiwa mzee vilevile?”+ 13 Kisha Yehova akamwambia Abrahamu: “Kwa nini Sara amecheka, akisema, ‘Je, kwa hakika na kwa kweli mimi nitazaa ingawa nimezeeka?’+ 14 Je, jambo lolote ni kubwa mno isivyo kawaida kwa Yehova?+ Kwa wakati uliowekwa nitarudi kwako, mwaka ujao wakati huu, na Sara atapata mwana.” 15 Lakini Sara akaanza kukana hilo, akisema: “Mimi sikucheka!” Kwa maana aliogopa. Ndipo yeye akasema: “Sivyo! ulicheka.”+

16 Baadaye hao wanaume wakasimama kutoka hapo wakatazama chini kuelekea Sodoma,+ naye Abrahamu alikuwa akitembea pamoja nao ili awasindikize.+ 17 Naye Yehova akasema: “Je, nimfiche Abrahamu jambo ninalofanya?+ 18 Tazama, kwa hakika Abrahamu atakuwa taifa kubwa na lenye nguvu, na mataifa yote ya dunia yatajibariki kupitia kwake.+ 19 Kwa maana nimefahamiana naye kusudi awaamuru wanawe na nyumba yake baada yake, ndipo washike njia ya Yehova ili kutenda uadilifu na haki;+ ili Yehova apate kumtimizia Abrahamu lile alilosema juu yake.”+

20 Ndipo Yehova akasema: “Kilio cha malalamiko juu ya Sodoma na Gomora+ ni kikubwa, na dhambi yao ni nzito sana.+ 21 Mimi nimeazimia kabisa kushuka ili nipate kuona kama wanatenda kabisa kulingana na kile kilio kilicho juu yake ambacho kimenifikia, na ikiwa sivyo, nitajua.”+

22 Basi wale wanaume wakageuka kutoka hapo, wakaenda Sodoma; lakini Yehova+ alikuwa bado amesimama mbele ya Abrahamu.+ 23 Kisha Abrahamu akakaribia na kuanza kusema: “Je, kweli utafagilia mbali mwadilifu pamoja na mwovu?+ 24 Tuseme kuna watu waadilifu 50 katika jiji hilo. Je, wewe, utawafagilia mbali, usisamehe mahali hapo kwa ajili ya wale waadilifu 50 ambao wamo ndani yake?+ 25 Ni jambo lisilowaziwa kwako kwamba unatenda namna hii kuua mtu mwadilifu pamoja na mwovu hivi kwamba mtu mwadilifu apatwe na jambo lilelile kama ilivyo kwa mwovu!+ Ni jambo lisilowaziwa kwako.+ Je, Mwamuzi wa dunia yote hatafanya lililo sawa?”+ 26 Kisha Yehova akasema: “Mimi nikipata katika Sodoma watu 50 waadilifu katika jiji hilo nitapasamehe mahali hapo pote kwa ajili yao.”+ 27 Lakini Abrahamu akaendelea kujibu na kusema: “Tafadhali, tazama nimejiamulia kusema na Yehova, hali mimi ni mavumbi na majivu.+ 28 Tuseme wale 50 walio waadilifu wapungue 5. Je, wewe utaliharibu jiji zima kwa kupungua hao 5?” Akajibu akasema: “Mimi sitaliharibu nikipata humo 45.”+

29 Lakini tena akasema zaidi naye, na kumwambia: “Tuseme 40 wapatikane humo.” Naye akamjibu: “Sitafanya hivyo kwa ajili ya wale 40.” 30 Lakini yeye akaendelea kusema: “Tafadhali, Yehova na asiwake hasira,+ bali acha niendelee kusema:+ Tuseme 30 wapatikane humo.” Naye akamjibu: “Mimi sitafanya hivyo nikipata 30 humo.” 31 Lakini yeye akaendelea kusema: “Tafadhali, tazama nimejiamulia mwenyewe kusema na Yehova:+ Tuseme 20 wapatikane humo.” Naye akamjibu: “Mimi sitaliharibu kwa ajili ya wale 20.”+ 32 Mwishowe yeye akasema: “Tafadhali, Yehova na asiwake hasira,+ bali acha niseme mara hii moja tu:+ Tuseme kumi wapatikane humo.” Naye akamjibu: “Mimi sitaliharibu kwa ajili ya hao kumi.”+ 33 Kisha Yehova+ akaenda zake alipokuwa amemaliza kusema na Abrahamu, naye Abrahamu akarudi kwake.

19 Basi wale malaika wawili wakafika Sodoma wakati wa jioni, na Loti alikuwa ameketi katika lango la Sodoma.+ Loti alipowaona, akasimama awapokee, akainama kifudifudi.+ 2 Naye akaanza kusema: “Tafadhali, sasa, bwana zangu, pitieni hapa, tafadhali, mwingie ndani ya nyumba ya mtumishi wenu, mkae usiku kucha, mwoshwe miguu yenu.+ Kisha mwamke mapema, msafiri na kwenda zenu.”+ Nao wakajibu wakasema: “Hapana, bali katika uwanja wa watu wote ndipo tutakapokaa usiku kucha.”+ 3 Lakini akawasisitizia sana,+ basi wakageuka na kuingia kwake, wakaingia ndani ya nyumba yake. Kisha akawafanyia karamu,+ akaoka keki zisizo na chachu,+ nao wakala.

4 Kabla hawajalala, wanaume wa jiji, wanaume wa Sodoma, wakaizingira nyumba,+ kuanzia mvulana mpaka mzee, watu wote wakiwa kikundi kimoja.+ 5 Nao wakaendelea kumwita Loti na kumwambia: “Wako wapi wale wanaume ambao waliingia kwako usiku wa leo? Walete nje kwetu ili tulale nao.”+

6 Mwishowe, Loti akawaendea nje kwenye mwingilio, lakini akaufunga mlango nyuma yake. 7 Kisha akasema: “Tafadhali, ndugu zangu, msitende vibaya.+ 8 Tafadhali, hapa nina binti wawili ambao hawajapata kamwe kulala na mwanamume.+ Tafadhali, acheni niwatoe nje kwenu. Kisha mwatendee kama ilivyo vema machoni penu.+ Ila tu wanaume hawa msiwatendee jambo,+ kwa kuwa ndiyo sababu wamekuja chini ya kivuli cha paa yangu.”+ 9 Nao wakajibu wakasema: “Toka hapa!” Nao wakaongeza hivi: “Mtu huyu aliye peke yake alikuja hapa kukaa akiwa mgeni+ na sasa anajifanya kuwa mwamuzi.+ Sasa sisi tutakutendea wewe vibaya zaidi kuliko wao.” Nao wakaja wakisongamana kwa nguvu juu ya huyo mwanamume,+ juu ya Loti, na walikuwa wakikaribia kuuvunja mlango.+ 10 Basi wale wanaume wakanyoosha mikono yao na kumwingiza Loti walimokuwa, ndani ya nyumba, nao wakaufunga mlango. 11 Lakini wakawapiga kwa upofu wanaume waliokuwa kwenye mwingilio wa nyumba,+ kuanzia aliye mdogo zaidi mpaka aliye mkubwa zaidi,+ hata wakawa wanajichosha wakijaribu kuutafuta mwingilio.+

12 Kisha hao wanaume wakamwambia Loti: “Je, una mtu yeyote mwingine hapa? Mwana-mkwe na wana wako na binti zako na wote walio wako jijini, watoe nje ya mahali hapa!+ 13 Kwa maana sisi tutapaharibu mahali hapa, kwa sababu kilio juu yao kimekuwa kikubwa mbele za Yehova,+ hivi kwamba Yehova alitutuma tuliharibu jiji.”+ 14 Kwa hiyo Loti akatoka nje akaanza kusema na wana-wakwe zake ambao wangechukua binti zake, naye akaendelea kusema: “Ondokeni! Tokeni mahali hapa, kwa sababu Yehova ataliharibu jiji!”+ Lakini machoni pa wana-wakwe zake alionekana kama mtu aliyekuwa anafanya mzaha.+

15 Hata hivyo, kulipopambazuka, malaika wakamhimiza Loti, wakisema: “Simama! Mchukue mke wako na binti zako wawili walio hapa,+ usije ukafagiliwa mbali katika makosa ya jiji hili!”+ 16 Alipoendelea kukawia,+ ndipo kwa huruma za Yehova kwake,+ wale wanaume wakaushika mkono wake na mkono wa mke wake na mikono ya binti zake wawili. Wakamtoa nje na kumweka nje ya jiji.+ 17 Ikawa kwamba, mara tu walipokuwa wamewatoa nje ya jiji, akaanza kusema: “Kimbia kwa ajili ya nafsi yako!+ Usitazame nyuma+ wala usisimame katika Wilaya yote!+ Kimbilia eneo lenye milima usije ukafagiliwa mbali!”+

18 Kisha Loti akawaambia: “Sivyo, tafadhali, Yehova! 19 Tafadhali, sasa, mtumishi wako amepata kibali machoni pako+ hivi kwamba unatukuza fadhili zako zenye upendo,+ fadhili ambazo umenionyesha ili kuhifadhi hai+ nafsi yangu, lakini mimi—mimi siwezi kukimbilia eneo lenye milima kwa sababu naogopa nisije nikafikiwa na msiba nife.+ 20 Tafadhali, sasa, jiji hili liko karibu kuweza kukimbiliwa nalo ni dogo.+ Tafadhali, acha nikimbilie huko—je, hilo si dogo?⁠—na nafsi yangu itaendelea kuishi.”+ 21 Kwa hiyo yeye akamwambia: “Haya, nakujali kwa kadiri hii pia+ kwa vile sitaliangamiza jiji ambalo umesema.+ 22 Fanya haraka! Kimbilia huko, kwa sababu mimi siwezi kufanya jambo lolote mpaka wewe utakapofika huko!”+ Ndiyo sababu aliliita jiji hilo Soari.+

23 Jua lilikuwa limetokeza juu ya nchi hiyo wakati Loti alipofika Soari.+ 24 Ndipo Yehova akanyesha kiberiti na moto kutoka kwa Yehova, kutoka mbinguni, juu ya Sodoma na juu ya Gomora.+ 25 Kwa hiyo akaendelea kuyaangamiza majiji hayo, hata Wilaya yote na wakaaji wote wa hayo majiji na mimea ya udongo.+ 26 Naye mke wake akaanza kutazama nyuma, akiwa nyuma yake, naye akawa nguzo ya chumvi.+

27 Sasa Abrahamu akaondoka asubuhi na mapema kwenda mahali alipokuwa amesimama mbele za Yehova.+ 28 Kisha akatazama chini kuelekea Sodoma na Gomora na kuelekea nchi yote ya Wilaya hiyo, akaona ajabu. Kumbe, tazama moshi mzito ulikuwa ukipanda kutoka nchi hiyo kama moshi mzito wa tanuru!+ 29 Ikawa kwamba Mungu alipoharibu majiji ya Wilaya hiyo, Mungu alimkumbuka Abrahamu, kwa kuwa alichukua hatua za kumwondoa Loti kutoka katikati ya hayo maangamizi alipokuwa akiyaangamiza majiji ambayo kati yake Loti alikuwa amekaa.+

30 Baadaye Loti akatoka Soari, akaanza kukaa pamoja na binti zake wawili katika eneo lenye milima,+ kwa sababu aliogopa kukaa Soari.+ Kwa hiyo yeye na binti zake wawili wakaanza kukaa pangoni. 31 Naye yule mzaliwa wa kwanza akamwambia yule mwanamke mdogo: “Baba yetu ni mzee na hakuna mwanamume yeyote katika nchi hii wa kulala nasi kulingana na njia ya dunia nzima.+ 32 Njoo, tumpe baba yetu divai anywe+ nasi tulale naye. Ndipo tuhifadhi uzao kutoka kwa baba yetu.”+

33 Basi wakaendelea kumpa baba yao divai anywe usiku huo;+ kisha mzaliwa wa kwanza akaingia ndani akalala na baba yake, lakini yeye hakujua wakati binti yake alipolala na wakati alipoamka. 34 Ikawa kwamba kesho yake mzaliwa wa kwanza akamwambia yule mdogo: “Haya, mimi nililala na baba yangu usiku wa jana. Tumpe divai anywe usiku wa leo pia. Kisha wewe uingie ndani ulale naye, ili tuhifadhi uzao kutoka kwa baba yetu.” 35 Kwa hiyo wakampa tena na tena baba yao divai anywe usiku huo pia; Kisha yule mdogo akaondoka, akalala naye, lakini yeye hakujua wakati binti yake alipolala na wakati alipoamka. 36 Na binti wote wawili wa Loti wakapata mimba kutoka kwa baba yao.+ 37 Baada ya muda yule mzaliwa wa kwanza akazaa mwana, akamwita jina lake Moabu.+ Yeye ndiye baba ya Moabu, mpaka leo hii.+ 38 Yule mdogo pia akazaa mwana. Akamwita jina lake Ben-ami. Yeye ndiye baba ya wana wa Amoni,+ mpaka leo hii.

20 Sasa Abrahamu akahamisha kambi kutoka huko+ mpaka nchi ya Negebu na kuanza kukaa katikati ya Kadeshi+ na Shuri+ na kukaa akiwa mgeni Gerari.+ 2 Na Abrahamu akasema tena kumhusu Sara mke wake: “Yeye ni dada yangu.”+ Basi Abimeleki mfalme wa Gerari akatuma watu, akamchukua Sara.+ 3 Baadaye Mungu akamjia Abimeleki katika ndoto ya usiku, akamwambia: “Tazama, wewe ni kama tu umekufa, kwa sababu ya mwanamke ambaye umemchukua,+ kwa kuwa yeye ni mke wa mwingine.”+ 4 Hata hivyo, Abimeleki hakuwa amemkaribia.+ Kwa hiyo akasema: “Yehova, je, utaua taifa ambalo kwa kweli ni lenye uadilifu?+ 5 Je, yeye hakuniambia, ‘Huyu ni dada yangu’? naye huyu—je, yeye pia hakusema, ‘Yeye ni ndugu yangu’? Mimi nimefanya jambo hili katika unyoofu wa moyo wangu na bila hatia mikononi mwangu.”+ 6 Basi Mungu wa kweli akamwambia katika ndoto: “Mimi pia nimejua kwamba katika unyoofu wa moyo wako umefanya hili,+ nami pia nilikuwa nikikuzuia usinitendee dhambi.+ Ndiyo sababu mimi sikukuruhusu umguse.+ 7 Lakini sasa mrudishe mke wa huyo mwanamume, kwa maana yeye ni nabii,+ naye atakuombea dua.+ Kwa hiyo uendelee kuishi. Lakini ikiwa humrudishi, jua kwamba utakufa hakika, wewe na wote walio wako.”+

8 Kwa hiyo Abimeleki akaamka asubuhi na mapema, akawaita watumishi wake wote na kuyasema mambo hayo yote masikioni mwao. Na watu hao wakaogopa sana. 9 Kisha Abimeleki akamwita Abrahamu na kumwambia: “Umetutendea nini, na ni dhambi gani nimekutendea, hata ukaleta juu yangu na ufalme wangu dhambi kubwa?+ Matendo ambayo hayakupaswa kutendwa, wewe umetenda kuhusiana nami.”+ 10 Na Abimeleki akaendelea kumwambia Abrahamu: “Ulikuwa na lengo gani kwa kufanya jambo hili?”+ 11 Abrahamu akajibu akasema: “Ni kwa sababu nilisema moyoni mwangu, ‘Bila shaka mahali hapa hawamwogopi Mungu.+ Nao hakika wataniua kwa sababu ya mke wangu.’+ 12 Na, tena, yeye kwa kweli ni dada yangu, ni binti ya baba yangu, ila tu si binti ya mama yangu; naye akawa mke wangu.+ 13 Ikawa kwamba, Mungu aliponihamisha kutoka katika nyumba ya baba yangu,+ ndipo nilipomwambia yeye, ‘Hizi ni fadhili zenye upendo+ unazoweza kunionyesha: Kila mahali ambako tutakwenda sema hivi kunihusu: “Yeye ni ndugu yangu.”’”+

14 Basi Abimeleki akachukua kondoo na ng’ombe na watumishi wanaume na wajakazi, akampa Abrahamu na kumrudishia mke wake Sara.+ 15 Tena Abimeleki akasema: “Tazama, nchi yangu iko wazi kwako. Kaa mahali ambapo ni pema machoni pako.”+ 16 Naye akamwambia Sara: “Tazama, mimi nampa ndugu yako+ vipande elfu moja vya pesa za fedha. Tazama, hizo zitakuwa kifuniko+ cha macho kwako kwa wote walio pamoja nawe, na mbele ya kila mtu, nawe umeondolewa shutuma.” 17 Naye Abrahamu akaanza kumwomba dua Mungu wa kweli;+ naye Mungu akamponya Abimeleki na mke wake na vijakazi wake, nao wakaanza kuzaa watoto. 18 Kwa maana Yehova alikuwa amefunga kabisa kila tumbo la uzazi la nyumba ya Abimeleki kwa sababu ya Sara, mke wa Abrahamu.+

21 Naye Yehova akamwelekezea Sara fikira kama alivyokuwa amesema, na sasa Yehova akamtendea Sara kama alivyokuwa amesema.+ 2 Naye Sara akapata mimba,+ kisha akamzalia Abrahamu mwana katika umri wake wa uzee kwa wakati uliowekwa ambao Mungu alikuwa amemwambia.+ 3 Basi Abrahamu akamwita mwana wake jina lake Isaka,+ aliyekuwa amezaliwa kwake, ambaye Sara alikuwa amemzalia. 4 Naye Abrahamu akamtahiri Isaka mwana wake akiwa na umri wa siku nane, kama Mungu alivyokuwa amemwamuru.+ 5 Naye Abrahamu alikuwa na umri wa miaka mia moja wakati Isaka mwana wake alipozaliwa. 6 Kisha Sara akasema: “Mungu amenitayarishia kicheko: kila mtu anayesikia hilo atanicheka.”+ 7 Naye akaongeza kusema: “Ni nani ambaye angemwambia Abrahamu, ‘Sara atanyonyesha watoto,’ maana nimezaa mwana katika umri wake wa uzee?”

8 Sasa huyo mtoto akaendelea kukua, akafikia kuachishwa kunyonya;+ na kisha Abrahamu akatayarisha karamu kubwa katika siku ya Isaka kuachishwa kunyonya. 9 Na Sara akawa anaona mwana wa Hagari Mmisri,+ ambaye alikuwa amemzalia Abrahamu, akidhihaki.+ 10 Kwa hiyo akaanza kumwambia Abrahamu: “Mfukuze kijakazi huyu na mwana wake, kwa maana mwana wa kijakazi huyu hatakuwa mrithi pamoja na mwanangu, Isaka!”+ 11 Lakini jambo hilo kuhusu mwana wake halikumpendeza Abrahamu hata kidogo.+ 12 Kisha Mungu akamwambia Abrahamu: “Usiruhusu jambo lolote ambalo Sara anazidi kukuambia liwe lisilokupendeza juu ya huyo mvulana na juu ya kijakazi wako. Sikiliza sauti yake, kwa sababu ule utakaoitwa uzao wako utakuwa kupitia Isaka.+ 13 Nami nitamfanya pia huyo mwana wa kijakazi+ kuwa taifa, kwa sababu yeye ni uzao wako.”+

14 Basi Abrahamu akaamka asubuhi na mapema, akachukua mkate na kiriba cha maji akampa Hagari,+ akakiweka juu ya bega lake, na yule mtoto,+ halafu akamruhusu aende. Naye akaenda zake, akatanga-tanga katika nyika ya Beer-sheba.+ 15 Mwishowe yale maji yakamalizika+ ndani ya kiriba, naye akamtupa+ mtoto chini ya mti mmoja. 16 Kisha akaenda mbele na kuketi chini peke yake, kama umbali wa mtupo wa upinde, kwa sababu alisema: “Acha mimi nisimwone mtoto anapokufa.”+ Kwa hiyo akaketi chini umbali fulani akaanza kupaaza sauti na kulia.+

17 Ndipo Mungu akaisikia sauti ya huyo mvulana,+ na malaika wa Mungu akamwita Hagari kutoka mbinguni na kumwambia:+ “Una nini, Hagari? Usiogope, kwa sababu Mungu amesikiliza sauti ya huyo mvulana pale alipo. 18 Simama, mwinue huyo mvulana, umshike kwa mkono wako, kwa sababu nitamfanya kuwa taifa kubwa.”+ 19 Kisha Mungu akafungua macho yake hata akaona kisima cha maji,+ naye akaenda, akaanza kukijaza maji kiriba na kumnywesha huyo mvulana. 20 Na Mungu akaendelea kuwa na huyo mvulana,+ naye akaendelea kukua na kukaa nyikani; naye akawa mpiga-mishale.+ 21 Naye akakaa katika nyika ya Parani,+ na mama yake akamchukulia mke kutoka nchi ya Misri.

22 Sasa ikawa wakati huo kwamba Abimeleki pamoja na Fikoli mkuu wa jeshi lake wakamwambia Abrahamu: “Mungu yuko pamoja nawe katika kila jambo unalofanya.+ 23 Basi sasa niapie hapa kwa Mungu+ kwamba hutanitendea kwa udanganyifu mimi na watoto wangu na wazao wangu;+ kwamba, kulingana na upendo mshikamanifu ambao nimekutendea,+ utanitendea mimi na nchi ambayo katika hiyo umekuwa ukikaa ukiwa mgeni.”+ 24 Kwa hiyo Abrahamu akasema: “Nitaapa.”+

25 Abrahamu alipomlaumu vikali Abimeleki kwa habari ya kisima cha maji ambacho watumishi wa Abimeleki walikuwa wamechukua kwa jeuri,+ 26 ndipo Abimeleki akasema: “Mimi sijui ni nani aliyefanya jambo hili, wala wewe mwenyewe hukuniambia hilo, wala mimi mwenyewe pia sijasikia hilo ila leo tu.”+ 27 Basi Abrahamu akachukua kondoo na ng’ombe akampa Abimeleki,+ na wote wawili wakafanya agano.+ 28 Abrahamu alipoweka kando wana-kondoo jike saba wa kundi, 29 Abimeleki akamwambia Abrahamu: “Hapa inamaanisha nini hawa wana-kondoo jike saba ambao umewaweka peke yao?” 30 Kisha akasema: “Wewe utakubali mkononi mwangu hao wana-kondoo jike saba kuwa ushahidi+ kwangu kwamba nimechimba kisima hiki.” 31 Hiyo ndiyo sababu aliita mahali hapo Beer-sheba,+ kwa sababu wote wawili walikuwa wamekula kiapo hapo. 32 Kwa hiyo wakafanya agano+ huko Beer-sheba, halafu Abimeleki akaisimama pamoja na Fikoli mkuu wa jeshi lake nao wakarudi mpaka nchi ya Wafilisti.+ 33 Kisha akapanda mkwaju huko Beer-sheba naye akaliitia hapo jina la Yehova,+ Mungu anayedumu mpaka wakati usio na kipimo.+ 34 Naye Abrahamu akaendelea kukaa siku nyingi akiwa mgeni katika nchi ya Wafilisti.+

22 Baada ya mambo hayo Mungu wa kweli akamjaribu Abrahamu.+ Kwa hiyo akamwambia: “Abrahamu!” naye akajibu, akasema: “Mimi hapa!”+ 2 Naye akaendelea kusema: “Tafadhali, mchukue mwana wako, mwana wako wa pekee unayempenda sana,+ Isaka,+ ufunge safari kwenda nchi ya Moria+ na huko umtoe kama toleo la kuteketezwa juu ya mmoja kati ya milima ambao nitakuonyesha.”+

3 Kwa hiyo Abrahamu akaamka asubuhi na mapema na kumtandika punda wake, akachukua wawili kati ya watumishi wake na Isaka mwana wake;+ naye akapasua kuni kwa ajili ya toleo la kuteketezwa. Kisha akaondoka, akafunga safari kwenda mahali ambapo Mungu wa kweli alimwonyesha. 4 Ilikuwa kwanza katika siku ya tatu kwamba Abrahamu aliinua macho yake akaanza kupaona mahali hapo kwa mbali. 5 Sasa Abrahamu akawaambia watumishi wake:+ “Ninyi kaeni hapa pamoja na punda, lakini mimi na huyu mvulana tunataka kwenda mbele huko tukaabudu,+ halafu tutarudi hapa mlipo.”

6 Baada ya hayo Abrahamu alichukua kuni za toleo la kuteketezwa akamtwika Isaka mwana wake,+ naye akachukua mikononi mwake moto na kisu cha kuchinjia, na wote wawili wakasonga mbele pamoja.+ 7 Na Isaka akaanza kumwambia Abrahamu baba yake: “Baba yangu!”+ Naye akasema: “Mimi hapa, mwanangu!”+ Basi akaendelea kusema: “Hapa pana moto na kuni, lakini yuko wapi kondoo kwa ajili ya toleo la kuteketezwa?”+ 8 Abrahamu akajibu akasema: “Mungu mwenyewe ataandaa kondoo wa toleo la kuteketezwa,+ mwanangu.” Na wote wawili wakaendelea kutembea pamoja.

9 Mwishowe wakafika mahali ambapo Mungu wa kweli alikuwa amemwonyesha, naye Abrahamu akajenga madhabahu+ hapo na kuziweka kuni kwa utaratibu, akamfunga Isaka mwana wake mikono na miguu na kumweka juu ya madhabahu juu ya zile kuni.+ 10 Kisha Abrahamu akanyoosha mkono wake akachukua kile kisu cha kuchinjia ili amuue mwana wake.+ 11 Lakini malaika wa Yehova akaanza kumwita kutoka mbinguni akisema:+ “Abrahamu, Abrahamu!” naye akajibu: “Mimi hapa!” 12 Naye akaendelea kusema: “Usinyooshe mkono wako juu ya huyo mvulana wala usimtendee jambo lolote kamwe,+ kwa maana sasa mimi najua kwamba wewe unamwogopa Mungu kwa kuwa hukunizuilia mwana wako, mwana wako wa pekee.”+ 13 Kisha Abrahamu akainua macho yake, akatazama na kumbe, kule mbele, kulikuwa na kondoo-dume aliyenaswa kwa pembe zake kichakani. Kwa hiyo Abrahamu akaenda, akamchukua huyo kondoo-dume, akamtoa kuwa toleo la kuteketezwa badala ya mwana wake.+ 14 Naye Abrahamu akaanza kuita jina la mahali hapo Yehova-yire. Ndiyo sababu leo kwa desturi husemwa: “Katika mlima wa Yehova itaandaliwa.”+

15 Na malaika wa Yehova akamwita Abrahamu mara ya pili kutoka mbinguni 16 akamwambia: “‘Naapa kwa nafsi yangu mwenyewe,’ asema Yehova,+ ‘kwamba kwa sababu ya uhakika wa kwamba wewe umefanya jambo hili nawe hukuzuia mwana wako, mwana wako wa pekee,+ 17 hakika nitakubariki nami nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni na kama chembe za mchanga zilizo kando ya bahari;+ na uzao wako utamiliki lango la adui zake.+ 18 Na kupitia kwa uzao wako+ mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki kwa sababu wewe umeisikiliza sauti yangu.’”+

19 Baada ya hayo Abrahamu akarudi kwa watumishi wake, nao wakasimama, wakaenda pamoja mpaka Beer-sheba.+ Abrahamu akaendelea kukaa Beer-sheba.

20 Basi ikawa kwamba baada ya mambo hayo habari ikamfikia Abrahamu: “Tazama, Milka+ pia amemzalia Nahori+ ndugu yako wana: 21 Usi mzaliwa wake wa kwanza na Buzi+ ndugu yake na Kemueli baba ya Aramu, 22 na Kesedi na Hazo na Pildashi na Yidlafu na Bethueli.”+ 23 Naye Bethueli akamzaa Rebeka.+ Hao wanane Milka alimzalia Nahori ndugu ya Abrahamu. 24 Kulikuwa na suria wake pia, ambaye jina lake lilikuwa Reuma. Baada ya muda yeye pia akazaa Teba na Gahamu na Tahashi na Maaka.+

23 Na maisha ya Sara yakawa miaka 127. Hiyo ndiyo iliyokuwa miaka ya maisha ya Sara.+ 2 Basi Sara akafa katika Kiriath-arba,+ yaani, Hebroni+ katika nchi ya Kanaani,+ naye Abrahamu akaingia ndani kumwombolezea Sara na kumlilia. 3 Kisha Abrahamu akaondoka mbele ya mfu wake akaanza kuongea na wana wa Hethi,+ akisema: 4 “Mimi ni mkaaji na mhamiaji katikati yenu.+ Nipeni mahali pangu pa kuzikia katikati yenu ili niweze kumzika mfu wangu kutoka machoni pangu.”+ 5 Basi wana wa Hethi wakamjibu Abrahamu, na kumwambia: 6 “Tusikilize, bwana wangu.+ Wewe ni mkuu katikati yetu, mtu wa Mungu.+ Katika mahali petu palipo bora kabisa pa kuzikia, zika mfu wako.+ Hakuna yeyote kati yetu atakayekunyima mahali pake pa kuzikia ili usizike mfu wako.”+

7 Basi Abrahamu akasimama, akawainamia hao wenyeji,+ wana wa Hethi,+ 8 na kuongea nao akisema: “Ikiwa nafsi zenu zinakubali kuzika mfu wangu kutoka machoni pangu, nisikilizeni na kumhimiza Efroni mwana wa Zohari kwa ajili yangu,+ 9 kwamba apate kunipa pango la Makpela,+ ambalo ni lake, lililo mwisho wa shamba lake. Na anipe hilo kati yenu kwa kiwango kamili cha fedha liwe mahali pangu pa kuzikia.”+

10 Basi, Efroni alikuwa amekaa kati ya wana wa Hethi. Kwa hiyo Efroni Mhiti+ akamjibu Abrahamu masikioni mwa wana wa Hethi pamoja na wale wote waliokuwa wakiingia lango la jiji, akisema:+ 11 “Hapana, bwana wangu! Nisikilize. Hilo shamba mimi nakupa wewe, na lile pango lililomo nakupa. Mbele ya macho ya wana wa watu wangu nakupa.+ Zika mfu wako.” 12 Kisha Abrahamu akainama mbele ya hao wenyeji 13 na kuongea na Efroni masikioni mwa hao wenyeji, akisema: “Laiti wewe—hapana, nisikilize! Mimi nitakupa kiwango cha fedha kwa ajili ya shamba hilo. Kichukue kutoka kwangu,+ ili nipate kumzika mfu wangu hapo.”

14 Kisha Efroni akamjibu Abrahamu, akimwambia hivi: 15 “Bwana wangu, nisikilize. Sehemu ya shamba yenye thamani ya shekeli za fedha mia nne, hiyo ni nini kati yangu na wewe? Kwa hiyo zika mfu wako.”+ 16 Naye Abrahamu akamsikiliza Efroni, na Abrahamu akampimia Efroni hicho kiwango cha fedha alichokuwa amesema masikioni mwa wana wa Hethi, shekeli za fedha mia nne zinazotumiwa na wanabiashara.+ 17 Kwa hiyo shamba la Efroni lililokuwa Makpela, iliyo mbele ya Mamre, lile shamba na lile pango lililokuwamo na miti yote iliyokuwa shambani,+ iliyokuwa ndani ya mipaka yake yote kuzunguka, ikathibitishiwa+ 18 Abrahamu kuwa mali yake iliyonunuliwa mbele ya macho ya wana wa Hethi kati ya wale wote wanaoingia katika lango la jiji lake.+ 19 Na baada ya hayo Abrahamu akamzika Sara mke wake katika pango la shamba la Makpela mbele ya Mamre, yaani, Hebroni, katika nchi ya Kanaani.+ 20 Hivyo lile shamba na lile pango lililokuwamo likathibitishiwa Abrahamu kuwa mahali pake pa kuzikia mikononi mwa wana wa Hethi.+

24 Abrahamu alikuwa mzee, amesonga katika miaka; na Yehova alikuwa amembariki Abrahamu katika kila jambo.+ 2 Kwa hiyo Abrahamu akamwambia mtumishi wake, yule mwenye umri mkubwa zaidi wa nyumbani mwake, aliyekuwa anasimamia vyote alivyokuwa navyo:+ “Tafadhali, weka mkono wako chini ya paja langu,+ 3 kwa kuwa lazima nikuapishe kwa Yehova,+ Mungu wa mbingu na Mungu wa dunia, kwamba hutamchukulia mwanangu mke kutoka kwa binti za Wakanaani ambao ninakaa kati yao,+ 4 bali utaenda mpaka nchi yangu na mpaka kwa watu wa jamaa yangu,+ nawe utamchukulia mwanangu, Isaka, mke.”

5 Lakini, huyo mtumishi akamwambia: “Itakuwaje ikiwa mwanamke huyo hataki kuja pamoja nami mpaka nchi hii? Je, ni lazima nihakikishe kwamba nimemrudisha mwana wako mpaka nchi ambayo wewe ulitoka?”+ 6 Abrahamu akajibu akamwambia: “Jihadhari usimrudishe mwanangu huko.+ 7 Yehova Mungu wa mbingu, aliyenichukua kutoka katika nyumba ya baba yangu na kutoka katika nchi ya watu wa jamaa yangu+ na ambaye alisema nami na ambaye aliniapia,+ akisema, ‘Nitaupa uzao wako+ nchi hii,’+ atatuma malaika wake mbele yako,+ nawe utachukua mke huko kwa ajili ya mwanangu.+ 8 Lakini ikiwa huyo mwanamke hataki kuja pamoja nawe, wewe pia utakuwa umewekwa huru kutoka kwenye kiapo hiki ulichonipa.+ Ila tu usimrudishe mwanangu huko.” 9 Basi huyo mtumishi akaweka mkono wake chini ya paja la Abrahamu bwana wake na kumwapia kuhusu jambo hilo.+

10 Basi huyo mtumishi akachukua ngamia kumi kutoka kwa ngamia za bwana wake, akatoka kwenda na kila namna ya kitu chema cha bwana wake mkononi mwake.+ Kisha akaondoka na kwenda Mesopotamia mpaka katika jiji la Nahori. 11 Mwishowe akafanya wale ngamia wapige magoti chini nje ya jiji kwenye kisima cha maji karibu na wakati wa jioni,+ karibu na wakati ambao wanawake wanaoteka maji walikuwa na desturi ya kutoka nje.+ 12 Naye akaendelea kusema: “Yehova Mungu wa bwana wangu Abrahamu,+ tafadhali, fanya hilo litukie mbele yangu leo nawe umfanyie bwana wangu Abrahamu+ fadhili zenye upendo.+ 13 Hapa nimesimama kwenye chemchemi ya maji, na binti za watu wa jiji wanatoka nje kuteka maji.+ 14 Litakalotokea ni kwamba mwanamke kijana ambaye nitamwambia, ‘Tafadhali, shusha mtungi wako wa maji ili ninywe,’ na ambaye kwa kweli atasema, ‘Kunywa, na pia nitanywesha ngamia zako,’ huyo ndiye utakayemchagulia mtumishi wako,+ Isaka; na kwa hilo unijulishe kwamba umefanya upendo mshikamanifu kwa bwana wangu.”+

15 Basi, ikawa kwamba kabla hajamaliza kusema,+ tazama, Rebeka, aliyezaliwa na Bethueli+ mwana wa Milka+ mke wa Nahori,+ ndugu ya Abrahamu, alikuwa akitoka nje na mtungi wake wa maji ukiwa begani mwake.+ 16 Sasa huyo mwanamke kijana alikuwa mwenye sura ya kuvutia sana,+ bikira, wala hakuna mwanamume aliyekuwa amelala naye.+ Akateremka kuja kwenye chemchemi, akaanza kujaza mtungi wake wa maji kisha akapanda. 17 Mara moja yule mtumishi akakimbia akutane naye na kusema: “Tafadhali, nipe maji kidogo katika mtungi wako.”+ 18 Naye akasema: “Kunywa, bwana wangu.” Kisha akashusha upesi mtungi wake mkononi mwake, akamnywesha.+ 19 Alipokuwa amemaliza kumnywesha, akasema: “Nitateka maji pia kwa ajili ya ngamia zako mpaka wamalize kunywa.”+ 20 Kwa hiyo akamimina upesi maji ya mtungi wake ndani ya chombo cha kunyweshea wanyama naye akakimbia tena na tena kisimani ili kuteka maji,+ akaendelea kuteka kwa ajili ya ngamia zake wote. 21 Wakati huo wote yule mwanamume alikuwa anamkazia macho kwa kustaajabu, akikaa kimya ili ajue ikiwa Yehova alikuwa amefanikisha safari yake au sivyo.+

22 Basi ikawa kwamba, wakati hao ngamia walipokuwa wamemaliza kunywa, yule mwanamume akachukua pete ya puani+ ya dhahabu yenye uzito wa nusu shekeli na vikuku+ viwili kwa ajili ya mikono yake, uzito wake ulikuwa shekeli kumi za dhahabu, 23 naye akasema: “Wewe ni binti ya nani? Tafadhali niambie. Je, mna nafasi yoyote nyumbani kwa baba yako tukae usiku huu?”+ 24 Akajibu akamwambia: “Mimi ni binti ya Bethueli+ mwana wa Milka, ambaye alimzalia Nahori.”+ 25 Naye akamwambia tena: “Tuna majani na chakula kingi cha mifugo, pia mahali pa kukaa usiku.”+ 26 Ndipo huyo mwanamume akainama chini akajilaza kifudifudi mbele za Yehova+ 27 na kusema: “Abarikiwe Yehova+ Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ambaye hakuacha fadhili zake zenye upendo na kuwa mwenye kutegemeka kumwelekea bwana wangu. Mimi nikiwa njiani, Yehova ameniongoza kwenye nyumba ya ndugu za bwana wangu.”+

28 Na yule mwanamke kijana akaenda mbio, akaambia nyumba ya mama yake juu ya mambo hayo. 29 Sasa Rebeka alikuwa na ndugu na jina lake lilikuwa Labani.+ Basi Labani akaenda mbio kwa yule mwanamume aliyekuwa nje kwenye chemchemi. 30 Ikawa kwamba alipoona ile pete ya puani na vikuku+ mikononi mwa dada yake na aliposikia maneno ya Rebeka dada yake, akisema: “Hivi ndivyo huyo mwanamume alivyosema nami,” ndipo akaja kwa huyo mwanamume na tazama alikuwa hapo, amesimama kando ya ngamia kwenye chemchemi. 31 Mara moja akasema: “Njoo, wewe mbarikiwa wa Yehova.+ Kwa nini unaendelea kusimama hapa nje, wakati mimi mwenyewe nimetayarisha nyumba na nafasi kwa ajili ya ngamia?” 32 Baada ya hayo, huyo mwanamume akaingia ndani ya nyumba, naye akaanza kufungua ngamia lijamu na kuwapa ngamia majani na chakula cha mifugo na maji ya kuosha miguu yake na miguu ya wanaume waliokuwa pamoja naye.+ 33 Kisha chakula kikawekwa mbele yake, lakini yeye akasema: “Mimi sitakula mpaka nitakapokuwa nimesema mambo yangu.” Kwa hiyo akamwambia: “Sema!”+

34 Kisha akaendelea kusema: “Mimi ni mtumishi wa Abrahamu.+ 35 Na Yehova amembariki bwana wangu sana kwa kuwa anaendelea kumfanya mkuu zaidi na kumpa kondoo na ng’ombe na fedha na dhahabu na watumishi wanaume na wajakazi na ngamia na punda.+ 36 Tena, Sara, mke wa bwana wangu alimzalia bwana wangu mwana baada ya kuzeeka;+ naye atampa kila kitu alicho nacho.+ 37 Kwa hiyo bwana wangu aliniapisha, akisema, ‘Usimchukulie mwanangu mke kutoka kwa binti za Wakanaani ambao ninakaa katika nchi yao.+ 38 Sivyo, bali utaenda kwenye nyumba ya baba yangu na kwa familia yangu+ nawe umchukulie mwanangu mke.’+ 39 Lakini nikamwambia bwana wangu, ‘Itakuwaje ikiwa mwanamke huyo hatakuja pamoja nami?’+ 40 Kisha akaniambia, ‘Yehova, ambaye mbele zake nimetembea,+ atatuma malaika+ wake pamoja nawe na kwa hakika atafanikisha njia yako;+ nawe umchukulie mwanangu mke kutoka kwa familia yangu na kutoka kwa nyumba ya baba yangu.+ 41 Wakati huo ndipo utakapoondolewa wajibu kwangu kwa kiapo unapofika kwa familia yangu, na ikiwa hawakupi mke, utakuwa bila wajibu kwangu kwa kiapo.’+

42 “Nilipofika kwenye chemchemi leo, ndipo nikasema, ‘Yehova Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ikiwa kwa kweli unafanikisha njia yangu ninayoiendea,+ 43 hapa mimi nimesimama kwenye chemchemi ya maji. Linalopaswa kutokea ni kwamba mwanamwali+ anayekuja nje kuteka maji ambaye kwa kweli nitamwambia: “Tafadhali, acha ninywe maji kidogo katika mtungi wako,” 44 na ambaye kwa kweli ataniambia: “Unywe wewe, nami pia nitateka maji kwa ajili ya ngamia zako,” yeye ndiye mwanamke ambaye Yehova amemchagulia mwana wa bwana wangu.’+

45 “Kabla sijamaliza kusema+ moyoni+ mwangu, tazama, Rebeka akatokea, pamoja na mtungi wake juu ya bega lake; naye akateremka mpaka kwenye chemchemi na kuanza kuteka maji.+ Ndipo nikamwambia, ‘Tafadhali, nipe maji.’+ 46 Kwa hiyo upesi akashusha mtungi wake kutoka kwake, akasema: ‘Kunywa,+ na pia nitanywesha ngamia zako.’ Kisha nikanywa, na pia akawanywesha ngamia. 47 Baada ya hayo nikamuuliza na kusema, ‘Wewe ni binti ya nani?’+ naye akasema, ‘Mimi ni binti ya Bethueli mwana wa Nahori, ambaye Milka alimzalia.’ Ndipo nikaweka pete katika pua yake na vikuku mikononi mwake.+ 48 Nami nikainama chini na kujilaza kifudifudi mbele za Yehova, nikambariki Yehova, Mungu wa bwana wangu Abrahamu,+ aliyekuwa ameniongoza katika njia ya kweli+ ili kuchukua binti ya ndugu ya bwana wangu kwa ajili ya mwana wake. 49 Na sasa ikiwa ninyi kwa kweli mnaonyesha fadhili zenye upendo na kuwa wenye kutegemeka kuelekea bwana wangu,+ niambieni; lakini ikiwa sivyo, niambieni, ili nipate kugeukia mkono wa kuume au wa kushoto.”+

50 Ndipo Labani na Bethueli wakajibu na kusema: “Jambo hili limetoka kwa Yehova.+ Sisi hatuwezi kukuambia baya wala jema.+ 51 Rebeka huyu mbele yako. Mchukue uende, na awe mke wa mwana wa bwana wako, kama vile ambavyo Yehova amesema.”+ 52 Ikawa kwamba mtumishi wa Abrahamu alipokuwa amesikia maneno yao, mara moja akajilaza kifudifudi chini mbele za Yehova.+ 53 Na huyo mtumishi akaanza kutoa vyombo vya fedha na vyombo vya dhahabu na mavazi akampa Rebeka; naye akawapa vitu bora ndugu yake na mama yake.+ 54 Baada ya hayo wakala na kunywa, yeye pamoja na wale wanaume waliokuwa pamoja naye, nao wakakaa hapo usiku huo, wakaamka asubuhi.

Kisha akasema: “Mniache niende kwa bwana wangu.”+ 55 Na ndugu yake na mama yake wakajibu wakasema: “Acha huyu mwanamke kijana akae pamoja nasi angalau kwa siku kumi. Baadaye anaweza kwenda.” 56 Lakini yeye akawaambia: “Msinizuilie, kwa kuwa Yehova amefanikisha njia yangu.+ Acheni niende, ili nipate kwenda kwa bwana wangu.”+ 57 Kwa hiyo wakasema: “Na tumwite huyo mwanamke kijana tusikie kutoka kinywani mwake.”+ 58 Kisha wakamwita Rebeka na kumwambia: “Je, wewe utaenda na mwanamume huyu?” Naye akasema: “Mimi niko tayari kwenda.”+

59 Basi wakamuaga Rebeka+ dada yao aende na mtunzaji wake+ na mtumishi wa Abrahamu na wanaume wake. 60 Nao wakaanza kumbariki Rebeka na kumwambia: “Ewe dada yetu, na uwe maelfu mara elfu kumi, na uzao wako na umiliki lango la wale wanaouchukia.”+ 61 Baada ya hayo Rebeka na watumishi wake wanawake+ wakaondoka wakaenda wakiwa wamepanda juu ya ngamia,+ wakimfuata yule mwanamume; na huyo mtumishi akamchukua Rebeka akaenda zake.

62 Sasa Isaka alikuwa amekuja kutoka njia inayoenda Beer-lahai-roi,+ kwa maana alikuwa anakaa katika nchi ya Negebu.+ 63 Na Isaka alikuwa nje akitembea ili atafakari+ shambani karibu na wakati wa jioni. Alipoinua macho yake na kutazama, kumbe, kule ngamia walikuwa wakija! 64 Rebeka alipoinua macho yake, akamwona Isaka, naye akaruka chini kutoka kwenye ngamia. 65 Kisha akamwambia yule mtumishi: “Yule mwanamume anayetembea pale shambani kuja kutupokea, ni nani?” naye mtumishi akasema: “Ni bwana wangu.” Naye Rebeka akachukua kitambaa cha kichwani, akajifunika.+ 66 Na yule mtumishi akaanza kumsimulia Isaka mambo yote aliyokuwa amefanya. 67 Baada ya hayo Isaka akamleta Rebeka ndani ya hema la Sara mama yake.+ Hivyo akamchukua Rebeka, naye akawa mke wake;+ naye akampenda,+ na Isaka akapata faraja baada ya kumpoteza mama yake.+

25 Kisha, kwa mara nyingine Abrahamu akachukua mke, naye aliitwa jina lake Ketura.+ 2 Baada ya muda akamzalia Zimrani na Yokshani na Medani na Midiani+ na Ishbaki na Shua.+

3 Yokshani akamzaa Sheba+ na Dedani.+

Na wana wa Dedani wakawa Ashurimu na Letushimu na Leumimu.

4 Na wana wa Midiani walikuwa Efa+ na Eferi na Hanoki na Abida na Eldaa.+

Wote hao walikuwa wana wa Ketura.

5 Baadaye Abrahamu alimpa Isaka kila kitu alichokuwa nacho,+ 6 lakini wana wa masuria ambao Abrahamu alikuwa nao Abrahamu aliwapa zawadi.+ Kisha alipokuwa bado hai, akawaagiza waende kutoka kwa Isaka mwana wake,+ upande wa mashariki, kwenye nchi ya Mashariki.+ 7 Na hizi ndizo siku za miaka ya maisha ya Abrahamu alizoishi, miaka 175. 8 Kisha Abrahamu akakata pumzi, akafa katika umri mwema wa uzee, akiwa mzee na mwenye kutosheka, naye akakusanywa kwa watu wake.+ 9 Basi Isaka na Ishmaeli wanawe wakamzika katika pango la Makpela katika shamba la Efroni mwana wa Zohari Mhiti lililoko mbele ya Mamre,+ 10 lile shamba ambalo Abrahamu alikuwa amenunua kutoka kwa wana wa Hethi. Hapo Abrahamu akazikwa, na pia Sara mke wake.+ 11 Ikatokea kwamba baada ya kifo cha Abrahamu, Mungu aliendelea kumbariki Isaka mwana wake,+ naye Isaka alikuwa akikaa karibu na Beer-lahai-roi.+

12 Na hii ndiyo historia ya Ishmaeli+ mwana wa Abrahamu ambaye Hagari Mmisri mjakazi wa Sara alimzalia Abrahamu.+

13 Basi haya ndiyo majina ya wana wa Ishmaeli, kufuatana na majina yao, kulingana na asili za familia zao: Mzaliwa wa kwanza wa Ishmaeli alikuwa Nebayothi+ na Kedari+ na Adbeeli na Mibsamu+ 14 na Mishma na Duma na Masa, 15 Hadadi+ na Tema,+ Yeturi, Nafishi na Kedema.+ 16 Hao ndio wana wa Ishmaeli, na hayo ndiyo majina yao kufuatana na nyua zao na kufuatana na kambi zao zilizozungushiwa kuta:+ wakuu kumi na wawili kulingana na ukoo wao.+ 17 Na hii ndiyo miaka ya maisha ya Ishmaeli, miaka 137. Kisha akakata pumzi, akafa. Akakusanywa kwa watu wake.+ 18 Nao wakaanza kukaa katika mahema tokea Havila+ karibu na Shuri,+ ambayo iko mbele ya Misri, mpaka Ashuru. Mbele ya ndugu zake wote alikaa.+

19 Na hii ndiyo historia ya Isaka mwana wa Abrahamu.+

Abrahamu akamzaa Isaka. 20 Na Isaka alikuwa na umri wa miaka 40 alipomchukua Rebeka binti ya Bethueli,+ Msiria,+ wa Padan-aramu, dada ya Labani Msiria, awe mke wake. 21 Naye Isaka akaendelea kumsihi Yehova hasa kwa ajili ya mke wake,+ kwa sababu alikuwa tasa;+ kwa hiyo Yehova akakubali kusihiwa kwa ajili yake,+ na Rebeka mke wake akapata mimba. 22 Na wale wana ndani yake wakaanza kupambana,+ hivi kwamba akasema: “Ikiwa hivi ndivyo ilivyo, hasa kwa nini niko hai?” Basi akaenda kumuuliza Yehova.+ 23 Naye Yehova akamwambia: “Mataifa mawili yamo tumboni mwako,+ na vikundi viwili vya mataifa vitatenganishwa kutoka tumboni mwako;+ na kikundi kimoja cha taifa kitakuwa chenye nguvu kuliko kile kingine,+ na mkubwa atamtumikia mdogo.”+

24 Mwishowe siku zake za kuzaa zikatimia, na, tazama! mapacha walikuwa tumboni mwake.+ 25 Kisha yule wa kwanza akatoka mwekundu kila mahali kama vazi rasmi la manyoya;+ kwa hiyo wakamwita jina lake Esau.+ 26 Na baadaye ndugu yake akatoka na mkono wake ulikuwa unashikilia kisigino cha Esau;+ kwa hiyo akaitwa jina lake Yakobo.+ Na Isaka alikuwa na umri wa miaka 60 wakati Rebeka alipowazaa.

27 Na wale wavulana wakawa wakubwa, naye Esau akawa mwanamume anayejua jinsi ya kuwinda,+ mwanamume wa mbugani, bali Yakobo akawa mwanamume asiye na lawama,+ akikaa katika mahema.+ 28 Na Isaka alimpenda Esau, kwa sababu ilimaanisha nyama ya mawindo kinywani mwake, lakini Rebeka alimpenda Yakobo.+ 29 Wakati mmoja Yakobo alikuwa anatokosa mchuzi, Esau alipofika kutoka mbugani naye alikuwa amechoka. 30 Kwa hiyo Esau akamwambia Yakobo: “Haraka, tafadhali, nipe nimeze chekundu—chekundu hicho, kwa maana nimechoka!” Hiyo ndiyo sababu jina lake lilikuwa Edomu.+ 31 Yakobo akajibu akasema: “Niuzie, kwanza kabisa, haki yako ya mzaliwa wa kwanza!”+ 32 Naye Esau akaendelea kusema: “Tazama mimi ninakaribia kufa, nayo haki ya kuzaliwa ina faida gani kwangu?” 33 Naye Yakobo akaongeza hivi: “Niapie kwanza kabisa!”+ Naye akamwapia, akamuuzia Yakobo haki yake ya mzaliwa wa kwanza.+ 34 Naye Yakobo akampa Esau mkate na mchuzi wa dengu, naye akala na kunywa.+ Kisha akaondoka akaenda zake. Kwa hiyo Esau aliidharau haki ya kuzaliwa.+

26 Basi kukatokea njaa katika nchi hiyo, mbali na ile njaa ya kwanza iliyotokea siku za Abrahamu,+ kwa hiyo Isaka akaenda kwa Abimeleki, mfalme wa Wafilisti, huko Gerari.+ 2 Ndipo Yehova akamtokea na kusema:+ “Usishuke kwenda Misri. Kaa katika nchi ambayo nitakuonyesha.+ 3 Kaa ukiwa mgeni katika nchi hii,+ nami nitaendelea kuwa pamoja nawe na kukubariki, kwa sababu nitakupa wewe na uzao wako nchi zote hizi,+ nami nitaitimiza ahadi yenye kiapo ambayo nilimwapia Abrahamu baba yako,+ 4 ‘Nami nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni. Nami nitaupa uzao wako nchi zote hizi;+ na kupitia uzao wako mataifa yote ya dunia yatajibariki,’+ 5 kwa sababu ya uhakika wa kwamba Abrahamu alisikiliza sauti yangu na kuendelea kushika wajibu wake kwangu, amri zangu, masharti yangu, na sheria zangu.”+ 6 Kwa hiyo Isaka akaendelea kukaa huko Gerari.+

7 Basi, wanaume wa mahali hapo wakawa wakiuliza juu ya mke wake, naye akawa akisema: “Yeye ni dada yangu.”+ Kwa maana aliogopa kusema “Ni mke wangu” kwa kuogopa kwamba, kama alivyosema, “wanaume wa mahali hapa wataniua kwa sababu ya Rebeka,” kwa sababu alikuwa mwenye sura ya kuvutia.+ 8 Basi, siku zake huko zilipoongezeka, Abimeleki, mfalme wa Wafilisti, alikuwa akiangalia nje dirishani na kutazama mazingira, na tazama, Isaka alikuwa anachezacheza pamoja na Rebeka mke wake.+ 9 Mara moja Abimeleki akamwita Isaka na kusema: “Kumbe, si mwingine bali ni mke wako! Kwa hiyo kwa nini ulisema, ‘Yeye ni dada yangu’?” Isaka akamjibu, akamwambia: “Nilisema hivyo kwa kuogopa nisije nikafa kwa sababu yake.”+ 10 Lakini Abimeleki akaendelea kusema: “Ni nini hili umetutendea sisi?+ Ilibaki kitambo kidogo tu na mmoja kati ya watu angelala na mke wako, nawe ungeleta hatia juu yetu!”+ 11 Ndipo Abimeleki akawaamuru watu wote, akisema: “Yeyote atakayemgusa mwanamume huyu na mke wake bila shaka atauawa!”

12 Baadaye Isaka akaanza kupanda mbegu katika nchi hiyo,+ na mwaka huo alikuwa akipata kufikia vipimo mia moja kwa kimoja,+ kwa kuwa Yehova alikuwa anambariki.+ 13 Basi huyo mwanamume akawa mkuu na kuendelea kusonga zaidi na zaidi na kuwa mkuu mpaka akawa mkuu sana.+ 14 Naye akaja kuwa na makundi ya kondoo na mifugo ya ng’ombe na kundi kubwa la watumishi,+ hivi kwamba Wafilisti wakaanza kumwonea wivu.+

15 Navyo visima vyote ambavyo watumishi wa baba yake walikuwa wamechimba siku za Abrahamu baba yake,+ Wafilisti wakawa wakivifunika na kuvijaza kwa udongo mkavu.+ 16 Mwishowe Abimeleki akamwambia Isaka: “Ondoka katika ujirani wetu, kwa sababu umepata nguvu mno kuliko sisi.”+ 17 Kwa hiyo Isaka akahama kutoka huko na kupiga kambi katika bonde la mto la Gerari+ na kuanza kukaa huko. 18 Naye Isaka akaanza tena kuchimba visima vya maji ambavyo walikuwa wamechimba siku za Abrahamu baba yake lakini ambavyo Wafilisti walikuwa wameviziba baada ya kifo cha Abrahamu;+ naye akaviita tena kwa majina yale ambayo baba yake alikuwa ameviita.+

19 Watumishi wa Isaka wakaendelea kuchimba katika bonde la mto na basi wakapata huko kisima cha maji safi. 20 Nao wachungaji wa Gerari wakaanza kugombana na wachungaji wa Isaka,+ wakisema: “Maji haya ni yetu!” Basi akakiita hicho kisima Eseki, kwa sababu walikuwa wameshindana naye. 21 Nao wakachimba kisima kingine, nao wakaanza kukigombania pia. Basi akakiita Sitna. 22 Baadaye akahama kutoka huko na kuchimba kisima kingine,+ lakini hawakukigombania. Basi akakiita Rehobothi na kusema: “Ni kwa sababu sasa Yehova ametupa sisi nafasi ya kutosha+ naye ametufanya tuongezeke duniani.”+

23 Kisha akapanda kutoka huko mpaka Beer-sheba.+ 24 Naye Yehova akamtokea usiku huo na kusema: “Mimi ni Mungu wa Abrahamu baba yako.+ Usiogope,+ kwa sababu mimi nipo pamoja nawe, nami nitakubariki wewe na kuuzidisha uzao wako kwa sababu ya Abrahamu mtumishi wangu.”+ 25 Basi akajenga madhabahu huko, akaliitia jina la Yehova+ na kupiga hema lake huko,+ na watumishi wa Isaka wakachimba kisima huko.

26 Baadaye Abimeleki akamjia kutoka Gerari pamoja na Ahuzathi rafiki yake wa karibu na Fikoli mkuu wa jeshi lake.+ 27 Basi Isaka akawaambia: “Kwa nini ninyi mmekuja kwangu, hali ninyi wenyewe mlinichukia na kwa sababu hiyo mkaniagiza nitoke katika ujirani wenu?”+ 28 Wakajibu, wakasema: “Bila shaka sisi tumeona kwamba Yehova amekuwa pamoja nawe.+ Hivyo tukasema, ‘Tafadhali, kiapo cha wajibu na kiwepo kati yetu,+ kati yetu na wewe, nasi na tufanye agano pamoja nawe,+ 29 kwamba wewe hutafanya lolote baya kutuelekea kama vile ambavyo sisi hatukukugusa wewe na kama vile ambavyo sisi tumetenda wema tu kukuelekea kwa kuwa tulikuagiza uende kwa amani.+ Wewe sasa ni mbarikiwa wa Yehova.’”+ 30 Kisha akawafanyia karamu nao wakala na kunywa.+ 31 Asubuhi iliyofuata waliamka mapema nao wakatoleana ahadi zenye kiapo.+ Baada ya hayo Isaka akawaacha waende zao nao wakaondoka kwake kwa amani.+

32 Ndipo siku hiyo ikatukia kwamba watumishi wa Isaka walikuja na kumpa habari kuhusu kisima ambacho walikuwa wamechimba,+ na kumwambia: “Tumepata maji!” 33 Hivyo akakiita Shiba. Hiyo ndiyo sababu jina la jiji hilo ni Beer-sheba+ mpaka leo hii.

34 Na Esau akafikia umri wa miaka 40. Kisha akamchukua Yudithi binti ya Beeri, Mhiti, kuwa mke na pia Basemathi binti ya Eloni, Mhiti.+ 35 Nao walikuwa chanzo cha uchungu wa roho kwa Isaka na Rebeka.+

27 Na ikawa kwamba Isaka alipokuwa mzee na macho yake yalikuwa yameingia giza mno asiweze kuona,+ akamwita Esau mwana wake mkubwa na kumwambia:+ “Mwanangu!” naye akamjibu: “Mimi hapa!” 2 Naye akaendelea kusema: “Tazama, mimi sasa nimekuwa mzee.+ Sijui siku ya kifo changu.+ 3 Kwa hiyo wakati huu chukua, tafadhali, vifaa vyako, podo lako na upinde wako, uende nje mbugani uniwindie mawindo fulani.+ 4 Kisha nifanyie chakula kitamu, kile ninachokipenda sana, halafu uniletee na, ah, acha nile, ili kwamba nafsi yangu ipate kukubariki wewe kabla ya kufa kwangu.”+

5 Hata hivyo, Rebeka alikuwa akisikiliza Isaka alipokuwa akisema na Esau mwana wake. Esau akaenda nje mbugani awinde mawindo ayalete.+ 6 Naye Rebeka akamwambia Yakobo mwana wake:+ “Tazama, mimi sasa hivi nimemsikia baba yako akimwambia Esau ndugu yako, akisema, 7 ‘Niletee mawindo fulani unifanyie chakula kitamu na, ah, acha nile, ili nipate kukubariki wewe mbele za Yehova kabla ya kifo changu.’+ 8 Na sasa, mwanangu, sikiliza sauti yangu katika lile ninalokuamuru.+ 9 Tafadhali nenda kundini uniletee kutoka humo wana-mbuzi wawili wazuri, ili nipate kuwatayarisha wawe chakula kitamu kwa ajili ya baba yako, chakula kile anachokipenda sana. 10 Kisha ukilete kwa baba yako naye apate kula, ili akubariki wewe kabla ya kifo chake.”

11 Naye Yakobo akamwambia Rebeka mama yake: “Lakini Esau ndugu yangu ni mwanamume mwenye nywele nyingi mwilini nami ni mwanamume mwenye ngozi laini.+ 12 Namna gani baba yangu akinipapasa?+ Ndipo hakika nitakuwa machoni pake kama mtu anayefanya mzaha,+ nami hakika nitajiletea laana wala si baraka.”+ 13 Ndipo mama yake akajibu, akamwambia: “Laana uliyokusudiwa wewe na iwe juu yangu, mwanangu.+ Ila tu sikiliza sauti yangu na uende, uniletee hao.”+ 14 Basi akaenda, akawapata, akawaleta kwa mama yake, naye mama yake akatayarisha chakula kitamu namna ambavyo baba yake alipenda sana. 15 Kisha Rebeka akachukua mavazi ya Esau mwana wake mkubwa,+ yale yenye kupendeza zaidi ambayo alikuwa nayo nyumbani,+ akamvika Yakobo mwana wake mdogo.+ 16 Akaweka ngozi za wana-mbuzi hao juu ya mikono yake na juu ya sehemu isiyo na nywele ya shingo yake.+ 17 Kisha akatia kile chakula kitamu na mkate aliokuwa ametayarisha mkononi mwa Yakobo mwana wake.+

18 Kwa hiyo akaingia ndani kwa baba yake na kusema: “Baba yangu!” naye akasema: “Mimi hapa! Wewe ni nani, mwanangu?” 19 Naye Yakobo akaendelea kumwambia baba yake: “Mimi ni Esau mzaliwa wako wa kwanza.+ Nimefanya kama vile ulivyoniambia. Inuka, tafadhali. Keti ule sehemu ya mawindo yangu, ndipo nafsi yako ipate kunibariki.”+ 20 Basi Isaka akamwambia mwana wake: “Imekuwaje kwamba umeyapata upesi sana, mwanangu?” Naye akasema: “Kwa sababu Yehova Mungu wako alifanya mawindo yakutane nami.” 21 Ndipo Isaka akamwambia Yakobo: “Tafadhali, njoo karibu ili nikupapase, mwanangu, nijue kama kwa kweli wewe ni mwanangu Esau au sivyo.”+ 22 Kwa hiyo Yakobo akamkaribia Isaka baba yake, naye akaanza kumpapasa, ndipo akasema: “Sauti ni sauti ya Yakobo, lakini mikono ni mikono ya Esau.”+ 23 Naye hakumtambua, kwa sababu mikono yake ilikuwa na nywele nyingi kama mikono ya Esau ndugu yake. Kwa hiyo akambariki.+

24 Baada ya hayo akasema: “Wewe kwa kweli ni mwanangu Esau?” naye akasema: “Ni mimi.”+ 25 Kisha akasema: “Leta karibu nami, nipate kula sehemu ya mawindo ya mwanangu, ndipo nafsi yangu ikubariki.”+ Basi akaleta karibu naye, naye akaanza kula, akaletewa divai naye akaanza kunywa. 26 Kisha Isaka baba yake akamwambia: “Njoo karibu, tafadhali, unibusu, mwanangu.”+ 27 Kwa hiyo akaja karibu akambusu, naye akanusa harufu ya mavazi yake.+ Naye akaanza kumbariki akisema:

“Tazama, harufu ya mwanangu ni kama harufu ya shamba ambalo Yehova amebariki. 28 Mungu wa kweli na akupe umande wa mbinguni+ na udongo wenye rutuba wa dunia+ na wingi wa nafaka na divai mpya.+ 29 Vikundi vya watu na vikutumikie na vikundi vya mataifa vikuinamie.+ Uwe bwana wa ndugu zako, na wana wa mama yako na wakuinamie.+ Na alaaniwe kila mmoja wa wale wanaokulaani, na abarikiwe kila mmoja wa wale wanaokubariki.”+

30 Basi ikawa mara tu Isaka alipokuwa amemaliza kumbariki Yakobo, ndiyo, kwa kweli ikawa hapo tu Yakobo alipokuwa ametoka mbele ya uso wa Isaka baba yake, Esau ndugu yake akarudi kutoka katika uwindaji wake.+ 31 Naye pia akaanza kutayarisha chakula kitamu. Kisha akakileta kwa baba yake na kumwambia baba yake: “Baba yangu na ainuke ale sehemu ya mawindo ya mwana wake, ndipo nafsi yako inibariki.”+ 32 Isaka, baba yake, akamjibu, akamwambia: “Wewe ni nani?” naye akasema: “Mimi ni mwana wako, mzaliwa wako wa kwanza, Esau.”+ 33 Naye Isaka akaanza kutetemeka kwa tetemeko kubwa sana, na kusema: “Ni nani, basi, aliyewinda mawindo akaja kuniletea, hivi kwamba nikala kila kitu kabla ya wewe kuingia nami nikambariki? Ndiyo, yeye pia atabarikiwa!”+

34 Aliposikia maneno ya baba yake, Esau akaanza kupaaza kilio kwa sauti kubwa na yenye uchungu na kumwambia baba yake:+ “Nibariki mimi, hata mimi pia, baba yangu!”+ 35 Lakini yeye akaendelea kusema: “Ndugu yako alikuja kwa udanganyifu ili aweze kupata baraka uliyokusudiwa.”+ 36 Akajibu, akasema: “Je, hiyo siyo sababu jina lake ni Yakobo, hivi kwamba anyakue mahali pangu mara mbili hizi?+ Haki yangu ya kuzaliwa tayari amechukua,+ na tazama wakati huu amechukua baraka yangu!”+ Kisha akaongeza: “Je, hukuniachia baraka yoyote?” 37 Lakini Isaka akamjibu Esau na kuendelea kusema: “Tazama nimemweka awe bwana juu yako,+ na ndugu zake wote nimempa kuwa watumishi,+ na nafaka na divai mpya nimetoa ili kumtegemeza,+ basi liko wapi lolote ninaloweza kukufanyia, mwanangu?”

38 Kisha Esau akamwambia baba yake: “Je, huna hata baraka moja tu, baba yangu? Nibariki mimi, hata mimi pia, baba yangu!”+ Kisha Esau akapaaza sauti yake na kuanza kulia machozi.+ 39 Basi Isaka baba yake akajibu, akamwambia:

“Tazama, makao yako yatakuwa mbali na udongo wenye rutuba wa dunia, na mbali na umande wa mbingu juu.+ 40 Nawe utaishi kwa upanga wako,+ na kumtumikia ndugu yako.+ Lakini itatokea kwamba, utakapokosa utulivu, wewe hakika utavunja nira yake kutoka shingoni pako.”+

41 Hata hivyo, Esau akaweka uadui kumwelekea Yakobo kwa sababu ya baraka ambayo baba yake alikuwa amembarikia,+ na Esau akaendelea kusema moyoni mwake:+ “Siku za kipindi cha kuomboleza baba yangu zinakaribia.+ Baada ya hizo nitamuua Yakobo ndugu yangu.”+ 42 Rebeka alipojulishwa maneno ya Esau mwana wake mkubwa, mara moja akapeleka habari na kumwita Yakobo mwana wake mdogo, akamwambia: “Tazama! Esau ndugu yako anajifariji kukuhusu—kukuua wewe.+ 43 Sasa, basi, mwanangu, sikiliza sauti yangu, ondoka,+ ukimbilie kwa Labani ndugu yangu huko Harani.+ 44 Nawe ukae naye kwa siku kadhaa mpaka ghadhabu ya ndugu yako itulie,+ 45 mpaka hasira ya ndugu yako igeukie mbali nawe, naye awe amesahau yale uliyomtendea.+ Nami kwa hakika nitapeleka habari nikuchukue kutoka huko. Kwa nini nifiwe pia na ninyi wawili siku moja?”

46 Baada ya hayo Rebeka akawa akimwambia Isaka: “Nimekuja kuyachukia sana haya maisha yangu kwa sababu ya binti za Hethi.+ Yakobo akichukua mke kutoka kwa binti za Hethi kama hawa kutoka kwa binti za hii nchi, basi maisha yana faida gani kwangu?”+

28 Basi Isaka akamwita Yakobo akambariki na kumwamuru akisema: “Usichukue mke kutoka kwa binti za Kanaani.+ 2 Ondoka, uende mpaka Padan-aramu kwa nyumba ya Bethueli baba ya mama yako na kutoka huko ujichukulie mke kati ya binti za Labani ndugu ya mama yako.+ 3 Na Mungu Mweza-Yote atakubariki na kukufanya uzae na kukuzidisha, nawe utakuwa kutaniko la vikundi vya watu.+ 4 Naye atakupa baraka ya Abrahamu,+ wewe na uzao wako pamoja nawe,+ ili upate kumiliki nchi ya makao yako ya kigeni,+ ambayo Mungu amempa Abrahamu.”+

5 Kwa hiyo Isaka akamwacha Yakobo aende, naye akafunga safari kwenda Padan-aramu, kwa Labani mwana wa Bethueli Msiria,+ ndugu ya Rebeka,+ mama ya Yakobo na Esau.+

6 Esau alipoona kwamba Isaka alikuwa amembariki Yakobo akamwacha aende Padan-aramu ajichukulie kutoka huko mke, na kwamba alipombariki aliweka juu yake amri, akisema: “Usichukue mke kati ya binti za Kanaani”;+ 7 na kwamba Yakobo alikuwa akimtii baba yake na mama yake naye alikuwa ameondoka kwenda Padan-aramu;+ 8 ndipo Esau akaona kwamba binti za Kanaani walikuwa wasiopendeza machoni pa Isaka baba yake.+ 9 Kwa hiyo Esau akaenda kwa Ishmaeli akamchukua Mahalathi binti ya Ishmaeli mwana wa Abrahamu, dada ya Nebayothi, kuwa mke wake, kuongezea wake zake wengine.+

10 Na Yakobo akazidi kwenda zake kutoka Beer-sheba, akaendelea mpaka Harani.+ 11 Mwishowe akafika mahali fulani, akaanza kukaa hapo usiku huo kwa sababu jua lilikuwa limetua. Kwa hiyo akachukua moja la mawe ya mahali hapo akaliweka kuwa kitu cha kutegemeza kichwa chake, akalala mahali hapo.+ 12 Naye akaanza kuota ndoto,+ na, tazama! kulikuwa na ngazi iliyosimamishwa juu ya dunia na kilele chake kilikuwa kimefika mbinguni; na, tazama! malaika za Mungu walikuwa wakipanda na kushuka juu yake.+ 13 Na, tazama! Yehova alikuwa amesimama juu yake, naye akaanza kusema:+

“Mimi ni Yehova Mungu wa Abrahamu baba yako na Mungu wa Isaka.+ Nchi ambayo unalala juu yake, nitakupa wewe na uzao wako.+ 14 Na uzao wako utakuwa kama chembe za mavumbi ya dunia,+ nawe hakika utaenea kotekote upande wa magharibi na wa mashariki na wa kaskazini na wa kusini,+ na kupitia kwako na kupitia kwa uzao wako familia zote za nchi hakika zitajibariki.+ 15 Na tazama, mimi nipo pamoja nawe, nami nitakutunza katika njia yote unayoenda, nami nitakurudisha kwenye nchi hii,+ kwa sababu sitakuacha mpaka niwe kwa kweli nimefanya hayo ambayo nimekuambia.”+

16 Kisha Yakobo akaamka katika usingizi wake, akasema: “Kwa kweli Yehova yupo mahali hapa na mimi mwenyewe sikujua hilo.” 17 Naye akaogopa, akaongeza kusema:+ “Jinsi mahali hapa panavyoogopesha!+ Bila shaka mahali hapa ni nyumba ya Mungu+ napo ndipo lango la mbinguni.” 18 Kwa hiyo Yakobo akaamka asubuhi na mapema, akachukua jiwe lililokuwa hapo kama kitu cha kutegemeza kichwa chake, naye akalisimamisha kama nguzo na kumimina mafuta juu yake.+ 19 Tena, akaita jina la mahali hapo Betheli,+ lakini ukweli ni kwamba, hapo zamani jina la jiji hilo lilikuwa ni Luzi.+

20 Ndipo Yakobo akaweka nadhiri,+ akisema: “Mungu akiendelea kuwa pamoja nami na kwa hakika anitunze katika njia hii ninayoiendea na kunipa mkate wa kula na mavazi ya kuvaa+ 21 nami hakika nirudi kwa amani nyumbani kwa baba yangu, basi Yehova atakuwa amejionyesha kuwa Mungu wangu.+ 22 Na jiwe hili ambalo nimesimamisha kuwa nguzo litakuwa nyumba ya Mungu,+ na katika kila kitu utakachonipa bila shaka nitakupa wewe sehemu ya kumi.”+

29 Kisha Yakobo akaanza mwendo, akasafiri kwenda nchi ya Watu wa Mashariki.+ 2 Basi akatazama, na hapo palikuwa na kisima shambani na tazama, makundi matatu ya kondoo yalikuwa yamelala chini hapo kando yake, kwa sababu walikuwa na desturi ya kunywesha maji makundi+ katika kisima hicho; na kulikuwa na jiwe kubwa juu ya kinywa cha hicho kisima.+ 3 Makundi yote yalipokuwa yamekusanywa hapo, waliviringisha jiwe kutoka kwenye kinywa cha kisima, nao wakanywesha makundi maji, kisha wakalirudisha jiwe mahali pake juu ya kinywa cha kisima.

4 Basi Yakobo akawaambia: “Ndugu zangu, mmetoka wapi?” nao wakasema: “Sisi tunatoka Harani.”+ 5 Ndipo akawaambia: “Je, mnamjua Labani+ mjukuu wa Nahori?”+ nao wakasema: “Tunamjua.” 6 Basi akawaambia: “Je, yeye hajambo?”+ Nao wakasema: “Hajambo. Na tazama, Raheli+ binti yake anakuja na kondoo!”+ 7 Naye akaendelea kusema: “Tazama, bado ni mchana sana. Sio wakati wa kukusanya mifugo. Wanywesheni maji kondoo, kisha mwende mwalishe.”+ 8 Wakajibu, wakasema: “Haturuhusiwi kufanya hivyo mpaka makundi yote yawe yamekusanywa nao kwa kweli wawe wameviringisha jiwe kutoka kwenye kinywa cha kisima. Ndipo tutakaponywesha kondoo maji.”

9 Alipokuwa bado anasema nao, Raheli+ akaja na kondoo wa baba yake, kwa maana alikuwa mchungaji.+ 10 Ikawa kwamba Yakobo alipomwona Raheli binti ya Labani ndugu ya mama yake na kondoo wa Labani ndugu ya mama yake, bila kukawia Yakobo akakaribia na kuliviringisha jiwe, akaliondoa kwenye kinywa cha hicho kisima na kuwanywesha maji kondoo wa Labani ndugu ya mama yake.+ 11 Kisha Yakobo akambusu+ Raheli, akapaaza sauti yake na kulia machozi.+ 12 Na Yakobo akaanza kumwambia Raheli kwamba yeye ni ndugu+ ya baba yake na kwamba yeye ni mwana wa Rebeka. Na Raheli akakimbia, akaenda kumwambia baba yake.+

13 Sasa ikawa kwamba mara tu Labani alipoisikia habari juu ya Yakobo mwana wa dada yake, akaanza kukimbia kwenda kumpokea.+ Kisha akamkumbatia na kumbusu, akamleta mpaka ndani ya nyumba yake.+ Naye akaanza kumsimulia Labani mambo hayo yote. 14 Baada ya hayo Labani akamwambia: “Wewe kwa kweli ni mfupa wangu na nyama yangu.”+ Basi akakaa naye mwezi mzima.

15 Kisha Labani akamwambia Yakobo: “Je, wewe ni ndugu yangu,+ na je, unitumikie bure?+ Niambie, Mshahara wako utakuwa nini?”+ 16 Basi, Labani alikuwa na binti wawili. Jina la yule mkubwa lilikuwa ni Lea+ na jina la yule mdogo Raheli. 17 Lakini macho ya Lea hayakuwa yaking’aa, bali Raheli+ alikuwa na umbo zuri na sura nzuri.+ 18 Naye Yakobo alimpenda Raheli. Kwa hiyo akasema: “Mimi niko tayari kukutumikia miaka saba kwa ajili ya Raheli binti yako mdogo.”+ 19 Labani akajibu akasema: “Ni afadhali nikupe wewe kuliko nimpe mwanamume mwingine.+ Endelea kukaa pamoja nami.” 20 Naye Yakobo akatumikia miaka saba kwa ajili ya Raheli,+ lakini machoni pake hiyo ikawa kama siku chache kwa sababu alimpenda.+

21 Kisha Yakobo akamwambia Labani: “Nipe mke wangu, kwa sababu siku zangu zimetimia, nawe uniruhusu nilale naye.”+ 22 Basi Labani akawakusanya watu wote wa mahali hapo, akafanya karamu.+ 23 Lakini ikawa kwamba wakati wa jioni akamchukua Lea binti yake, akamleta kwa Yakobo ili apate kulala naye. 24 Pia, Labani akampa Lea binti yake mjakazi wake Zilpa,+ awe mjakazi wake. 25 Basi kufika asubuhi akakuta kumbe ni Lea! Kwa hiyo akamwambia Labani: “Ni nini hili umenitendea? Je, sikukutumikia kwa ajili ya Raheli? Basi kwa nini umenifanyia ujanja?”+ 26 Labani akajibu akasema: “Si desturi kufanya hivi kwetu, kumtoa mwanamke mdogo kabla ya mzaliwa wa kwanza. 27 Sherehekea+ kikamili juma la mwanamke huyu. Baadaye utapewa pia mwanamke huyu mwingine kwa utumishi ambao wewe unaweza kunitumikia kwa miaka saba zaidi.”+ 28 Basi Yakobo akafanya hivyo, akasherehekea kikamili juma la mwanamke huyo, baada ya hayo akampa Raheli binti yake kuwa mke wake. 29 Tena, Labani akampa Raheli binti yake Bilha+ mjakazi wake, awe mjakazi wake.

30 Kisha akalala na Raheli pia, naye akamwonyesha Raheli upendo zaidi kuliko Lea,+ naye akamtumikia Labani kwa miaka saba zaidi.+ 31 Yehova alipoona kwamba Lea alichukiwa, ndipo akafungua tumbo lake la uzazi,+ lakini Raheli alikuwa tasa.+ 32 Basi Lea akapata mimba, akazaa mwana na kisha akamwita jina lake Rubeni,+ kwa maana alisema: “Ni kwa sababu Yehova ametazama taabu yangu,+ kwa kuwa sasa mume wangu ataanza kunipenda.” 33 Naye akapata mimba tena, akazaa mwana kisha akasema: “Ni kwa sababu Yehova amesikiliza,+ kwa kuwa nilichukiwa na kwa hiyo akanipa huyu pia.” Ndipo akamwita jina lake Simeoni.+ 34 Naye akapata mimba tena, akazaa mwana kisha akasema: “Sasa wakati huu mume wangu atajiunga nami, kwa sababu nimemzalia wana watatu.” Kwa hiyo akaitwa jina lake Lawi.+ 35 Naye akapata mimba tena, akazaa mwana kisha akasema: “Mara hii nitamsifu Yehova.” Kwa hiyo akamwita jina lake Yuda.+ Kisha akaacha kuzaa.

30 Raheli alipoona kwamba alikuwa hajamzalia Yakobo mwana yeyote, Raheli akamwonea wivu dada yake naye akaanza kumwambia Yakobo:+ “Nipe watoto, kama sivyo nitakufa mimi.”+ 2 Kwa hiyo hasira ya Yakobo ikawaka juu ya Raheli naye akasema:+ “Je, mimi niko badala ya Mungu, ambaye amekuzuilia uzao wa tumbo?”+ 3 Basi yeye akasema: “Kijakazi wangu Bilha+ huyu. Lala naye, apate kuzaa magotini pangu ili kwamba mimi, naam mimi, nipate watoto kwake.”+ 4 Basi akampa Bilha mjakazi wake awe mke na Yakobo akalala naye.+ 5 Na Bilha akapata mimba na baada ya muda akamzalia Yakobo mwana.+ 6 Ndipo Raheli akasema: “Mungu ametenda kama mwamuzi+ wangu na pia ameisikiliza sauti yangu, akanipa mwana.” Ndiyo sababu alimwita jina lake Dani.+ 7 Na Bilha, mjakazi wa Raheli, akapata mimba mara nyingine tena, na baada ya muda akamzalia Yakobo mwana wa pili. 8 Kisha Raheli akasema: “Nimepigana miereka yenye nguvu na dada yangu. Nami nimekuwa mshindi!” Kwa hiyo akamwita jina lake Naftali.+

9 Lea alipoona kwamba ameacha kuzaa, akamchukua Zilpa mjakazi wake akampa Yakobo kuwa mke.+ 10 Baada ya muda Zilpa, mjakazi wa Lea, akamzalia Yakobo mwana. 11 Ndipo Lea akasema: “Neema!” Basi akamwita jina lake Gadi.+ 12 Baada ya hayo, Zilpa, mjakazi wa Lea, akamzalia Yakobo mwana wa pili. 13 Kisha Lea akasema: “Pamoja na furaha yangu! Kwa maana binti watanitangaza kuwa mwenye furaha.”+ Basi akamwita jina lake Asheri.+

14 Ndipo Rubeni+ akaenda kutembea siku za mavuno ya ngano,+ akapata dudai shambani. Kwa hiyo akazileta kwa Lea mama yake. Kisha Raheli akamwambia Lea: “Tafadhali, nipe baadhi ya dudai za mwana wako.”+ 15 Akajibu akamwambia: “Je, hili ni jambo dogo, kwamba wewe umemchukua mume wangu,+ na sasa wewe uzichukue pia dudai za mwanangu?” Basi Raheli akasema: “Kwa sababu hiyo yeye atalala nawe usiku wa leo kwa kubadilishana na dudai za mwana wako.”

16 Yakobo alipokuwa akitoka shambani jioni,+ Lea akaenda kumpokea kisha akasema: “Utalala nami, kwa sababu nimekukodi moja kwa moja kwa dudai za mwanangu.” Basi akalala naye usiku huo.+ 17 Basi Mungu akamsikia na kumjibu Lea naye akapata mimba na baada ya muda akamzalia Yakobo mwana wa tano.+ 18 Kisha Lea akasema: “Mungu amenipa mshahara wa mtu wa kukodiwa, kwa sababu nimempa mume wangu mjakazi wangu.” Kwa hiyo akamwita jina lake Isakari.+ 19 Lea akapata mimba mara nyingine tena na baada ya muda akamzalia Yakobo mwana wa sita.+ 20 Ndipo Lea akasema: “Mungu amenipa kipawa, ndiyo, kipawa chema. Mwishowe mume wangu atanivumilia,+ kwa sababu nimemzalia wana sita.”+ Basi akamwita jina lake Zabuloni.+ 21 Na baadaye akazaa binti kisha akamwita jina lake Dina.+

22 Mwishowe Mungu akamkumbuka Raheli, naye Mungu akamsikia na kumjibu kwa kuwa alifungua tumbo lake la uzazi.+ 23 Naye akapata mimba, akazaa mwana. Kisha akasema: “Mungu ameondolea mbali shutuma yangu!”+ 24 Basi akamwita jina lake Yosefu,+ akisema: “Yehova ananiongezea mwana mwingine.”

25 Ikawa kwamba Raheli alipokuwa amemzaa Yosefu, bila kukawia Yakobo akamwambia Labani: “Niruhusu niende kwangu na katika nchi yangu.+ 26 Nipe wake zangu na watoto wangu, ambao kwa ajili yao nimekutumikia, ili nipate kwenda; kwa maana wewe mwenyewe unajua utumishi wangu ambao nimekutolea.”+ 27 Ndipo Labani akamwambia: “Ikiwa, sasa, nimepata kibali machoni pako,—nimezifasiri zile ishara za bahati zinazoonyesha kwamba Yehova ananibariki kwa ajili yako.”+ 28 Naye akaongezea kusema: “Niambie masharti ya mshahara wako nami nitayatimiza.”+ 29 Basi akamwambia hivi: “Wewe mwenyewe unajua jinsi nimekutumikia na jinsi hali ya mifugo yako imekuwa mkononi mwangu;+ 30 kwamba kwa kweli ulikuwa na kidogo kabla ya kuja kwangu, nayo ikaendelea kuongezeka na kuwa mingi, kwa kuwa Yehova alikubariki tangu nilipoingia.+ Basi sasa ni wakati gani mimi nitafanya jambo pia kwa ajili ya nyumba yangu mwenyewe?”+

31 Kisha akasema: “Nikupe nini?” Naye Yakobo akaendelea kusema: “Hutanipa chochote kamwe!+ Ukinitendea jambo hili, mimi nitaanza tena kuchunga kundi lako.+ Nitaendelea kulilinda.+ 32 Mimi nitapita kati ya kundi lako lote leo. Wewe uweke kando kutoka hapo kila kondoo mwenye mabaka na mwenye madoa-doa ya rangi, na kila kondoo mwenye rangi ya kahawia kati ya wana-kondoo dume na yeyote kati ya mbuzi-jike mwenye madoa-doa ya rangi na mabaka. Baada ya hapo hao wawe mshahara wangu.+ 33 Na wema wangu niliotenda utanitetea siku yoyote ya baadaye ambayo huenda ukaja kuutazama mshahara wangu;+ kila mmoja asiye na mabaka na madoa-doa ya rangi kati ya mbuzi-jike na rangi ya kahawia kati ya wana-kondoo dume ni kitu kilichoibwa ikiwa yupo pamoja nami.”+

34 Labani akajibu akasema: “Ni vema! Na iwe kulingana na neno lako.”+ 35 Kisha akaweka kando siku hiyo mbuzi-dume wenye mistari-mistari na madoa-doa ya rangi na mbuzi-jike wote wenye mabaka na madoa-doa ya rangi, kila mmoja kati ya wana-kondoo dume aliyekuwa na weupe wowote na kila mmoja wa rangi ya kahawia, lakini akawatia mikononi mwa wanawe. 36 Baada ya hayo akaenda kukaa umbali wa safari ya siku tatu kati yake na Yakobo, na Yakobo alikuwa akichunga mifugo ya Labani iliyobaki.

37 Kisha Yakobo akachukua fimbo zilizokuwa bado mbichi za mlubna+ na za mlozi+ na za mwaramoni ili azitumie,+ akaziambua madoa meupe kwa kumenya sehemu nyeupe-nyeupe zilizokuwa kwenye hizo fimbo.+ 38 Mwishowe zile fimbo alizokuwa amezimenya akaziweka mbele ya kundi, katika mifereji, katika vyombo vya kunyweshea wanyama,+ ambapo makundi wangekuja kunywa, ili wapate kupandana mbele yazo walipokuja kunywa.

39 Basi hayo makundi yalikuwa yakipata hamu ya kupandana mbele ya hizo fimbo, nayo makundi yalikuwa yakizaa wenye mistari-mistari, wenye mabaka na wenye madoa-doa ya rangi.+ 40 Naye Yakobo akatenganisha wale wana-kondoo dume kisha akageuza nyuso za makundi kuelekea wale wenye mistari-mistari na wote wa rangi ya kahawia kati ya makundi ya Labani. Halafu akaweka makundi yake mwenyewe peke yake wala hakuwaweka kando ya mifugo ya Labani. 41 Ikawa sikuzote kwamba wakati wowote ambao makundi yenye nguvu+ yalikuwa tayari kupandana, Yakobo alikuwa akiweka hizo fimbo katika michirizi+ mbele ya macho ya makundi, ili wapate hamu ya kupandana kando ya hizo fimbo. 42 Lakini makundi hayo yalipoonyesha unyonge hakuyaweka hapo. Kwa hiyo wanyonge sikuzote wakawa wa Labani, lakini wenye nguvu wakawa wa Yakobo.+

43 Na huyo mwanamume akaendelea kuongezeka zaidi na zaidi, akawa na makundi makubwa na wajakazi na watumishi wanaume na ngamia na punda.+

31 Baadaye akasikia maneno ya wana wa Labani, wakisema: “Yakobo amechukua kila kitu kilichokuwa cha baba yetu; naye amekusanya mali hii yote kutoka kwa mali iliyokuwa ya baba.”+ 2 Wakati Yakobo alipokuwa akiutazama-tazama uso wa Labani, tazama haukuwa pamoja naye kama hapo zamani.+ 3 Mwishowe Yehova akamwambia Yakobo: “Rudi kwenye nchi ya baba zako na kwa watu wa jamaa yako,+ nami nitaendelea kuwa pamoja nawe.”+ 4 Kisha Yakobo akatuma ujumbe Raheli na Lea waitwe waje shambani kwenye kundi lake, 5 naye akawaambia:

“Ninaona uso wa baba yenu, kwamba yeye si yuleyule kunielekea kama hapo zamani;+ lakini Mungu wa baba yangu amekuwa pamoja nami.+ 6 Nanyi wenyewe mnajua kwa hakika kwamba nimemtumikia baba yenu kwa nguvu zangu zote.+ 7 Baba yenu amenichezea, naye amebadili mshahara wangu mara kumi, lakini Mungu hakumruhusu anidhuru.+ 8 Ikiwa kwa upande mmoja alisema, ‘Wenye mabaka watakuwa mshahara wako,’ ndipo kundi zima lilizaa wenye mabaka; lakini ikiwa kwa upande mwingine alisema, ‘Wenye mistari-mistari watakuwa mshahara wako,’ ndipo kundi zima lilizaa wenye mistari-mistari.+ 9 Kwa hiyo Mungu akazidi kuchukua mifugo ya baba yenu na kunipa mimi.+ 10 Mwishowe ikawa kwamba kundi lilipokuwa na hamu ya kupandana nikainua macho yangu nikaona maono katika ndoto+ na tazama, mbuzi-dume wanaopanda kundi walikuwa wenye mistari-mistari, wenye mabaka na madoa-doa.+ 11 Kisha malaika wa Mungu wa kweli akaniambia katika ndoto, ‘Yakobo!’ nikajibu nikasema, ‘Mimi hapa.’+ 12 Naye akaendelea kusema, ‘Inua macho yako, tafadhali, uone mbuzi-dume wote wanaopanda kundi ni wenye mistari-mistari, mabaka na madoa-doa, kwa maana nimeona yote ambayo Labani anakutendea.+ 13 Mimi ndimi Mungu wa kweli wa Betheli,+ ambapo ulitia mafuta nguzo+ na ambapo uliniwekea nadhiri.+ Basi ondoka, toka katika nchi hii urudi kwenye nchi ya kuzaliwa kwako.’”+

14 Ndipo Raheli na Lea wakajibu na kumwambia: “Je, kungali na fungu la urithi tena kwa ajili yetu katika nyumba ya baba yetu?+ 15 Je, kwa kweli sisi hatuonwi kuwa wageni kwake kwa kuwa yeye ametuuza, hivi kwamba anaendelea kula sikuzote kutokana na pesa zilizotolewa kwa ajili yetu?+ 16 Kwa maana utajiri wote ambao Mungu amechukua kutoka kwa baba yetu ni wetu na wa watoto wetu.+ Basi sasa kila jambo ambalo Mungu amekuambia, fanya.”+

17 Kisha Yakobo akaondoka, akawapandisha watoto wake na wake zake juu ya ngamia;+ 18 naye akaanza kupeleka mifugo yake yote na mali zote ambazo alikuwa amekusanya,+ mifugo ya mapato yake ambayo alikuwa amekusanya Padan-aramu, ili aende kwa Isaka baba yake katika nchi ya Kanaani.+

19 Sasa Labani alikuwa ameenda kunyoa kondoo wake. Wakati huohuo Raheli aliiba terafimu+ zilizokuwa za baba yake. 20 Kwa hiyo Yakobo akamshinda akili Labani, Msiria, kwa sababu hakuwa amemwambia kwamba atakimbia. 21 Naye akakimbia, akaondoka na kuvuka ule Mto,+ yeye na vyote alivyokuwa navyo. Baada ya hapo akaelekeza uso wake kwenye eneo lenye milima la Gileadi.+ 22 Baadaye, siku ya tatu, Labani aliambiwa kwamba Yakobo alikuwa amekimbia. 23 Basi akachukua ndugu zake pamoja naye akaanza kumfuatilia+ mwendo wa safari ya siku saba, akamfikia katika eneo lenye milima la Gileadi. 24 Ndipo Mungu akamjia Labani Msiria+ katika ndoto wakati wa usiku+ na kumwambia: “Jiangalie usije ukamwambia Yakobo jema wala baya.”+

25 Basi Labani akamkaribia Yakobo, kwa kuwa Yakobo alikuwa amepiga hema mlimani na Labani alikuwa amepiga kambi kwa ajili ya ndugu zake katika eneo lenye milima la Gileadi. 26 Ndipo Labani akamwambia Yakobo: “Umefanya nini, kwa kuwa ulinishinda akili na kupeleka binti zangu kama mateka waliochukuliwa kwa upanga?+ 27 Kwa nini ukakimbia kisiri na kunishinda akili wala usiniambie, ili nipate kukuaga kwa shangwe na kwa nyimbo,+ kwa tari na kwa kinubi?+ 28 Nawe hukunipa nafasi ya kuwabusu watoto wangu na binti zangu.+ Basi umetenda kipumbavu. 29 Mkono wangu una nguvu za kuwatendea ninyi mabaya,+ lakini Mungu wa baba yenu aliongea nami usiku uliopita, akisema, ‘Jiangalie usije ukamwambia Yakobo jema wala baya.’+ 30 Ingawa wewe kwa kweli umeenda sasa kwa sababu umekuwa ukitamani mno nyumba ya baba yako, hata hivyo, kwa nini umeiba miungu yangu?”+

31 Yakobo akajibu, akamwambia Labani: “Ni kwa sababu niliogopa.+ Kwa maana nilisema moyoni mwangu, ‘Unaweza kuninyang’anya binti zako.’ 32 Yeyote yule ambaye huenda ukampata akiwa na miungu yako, asiishi.+ Mbele ya ndugu zetu, chunguza mwenyewe kile kilicho pamoja nami na uichukue.”+ Lakini Yakobo hakujua kwamba Raheli alikuwa ameiiba.+ 33 Kwa hiyo Labani akaingia katika hema la Yakobo na hema la Lea na hema la wale vijakazi wawili,+ lakini hakuipata. Mwishowe akatoka katika hema la Lea akaenda katika hema la Raheli. 34 Basi Raheli alikuwa amechukua hizo terafimu, naye akaziweka katika kikapu cha matandiko ya kukaliwa na mwanamke juu ya ngamia, naye akaendelea kuzikalia. Basi Labani akakagua hema lote, lakini hakuzipata. 35 Ndipo Raheli akamwambia baba yake: “Hasira isiwake machoni pa bwana wangu,+ kwa sababu mimi siwezi kusimama mbele yako, kwa maana nimepatwa na kilicho desturi kwa wanawake.”+ Kwa hiyo akaendelea kutafuta kwa uangalifu, lakini hakuzipata hizo terafimu.+

36 Naye Yakobo akakasirika,+ akaanza ugomvi na Labani, na Yakobo akajibu na kumwambia Labani: “Kuna maasi gani upande wangu,+ ni nini dhambi yangu, iwe ndiyo sababu umenifuatilia vikali?+ 37 Sasa kwa kuwa umekagua mali zangu zote, kati ya mali zote za nyumba yako umepata nini?+ Kiweke hapa mbele ya ndugu zangu na ndugu zako,+ uwaache waamue kati yetu wawili.+ 38 Miaka hii 20 nimekuwa pamoja nawe. Kondoo-jike zako na mbuzi-jike zako hawakutokwa na mimba,+ na kondoo-dume wa kundi lako sikuwala kamwe. 39 Mnyama yeyote aliyeraruliwa vipande-vipande sikukuletea.+ Mimi mwenyewe nililipa hasara yake. Iwe mmoja aliibwa wakati wa mchana au aliibwa wakati wa usiku, wewe ulimtaka mkononi mwangu.+ 40 Nimejionea kwamba wakati wa mchana joto limenimaliza nguvu, na baridi wakati wa usiku, nao usingizi wangu ulikimbia machoni pangu.+ 41 Nina jumla ya miaka 20 nyumbani kwako. Mimi nimekutumikia miaka 14 kwa ajili ya binti zako wawili na miaka 6 kwa ajili ya kundi lako, nawe ulizidi kubadili mshahara wangu mara kumi.+ 42 Kama Mungu wa baba yangu,+ Mungu wa Abrahamu na aliye Hofu ya Isaka,+ hangekuwa upande wangu, wewe ungeniacha sasa niende zangu nikiwa mikono mitupu. Taabu na kazi ya mikono yangu Mungu ameona, na kwa hiyo akakukaripia usiku uliopita.”+

43 Ndipo Labani akajibu, akamwambia Yakobo: “Binti hawa ni binti zangu na watoto hawa ni watoto wangu na kundi hili ni kundi langu, na kila kitu unachokitazama ni changu na cha binti zangu. Ni nini ninachoweza kuwatendea hawa leo au watoto wao ambao wamezaa? 44 Na sasa, njoo tufanye agano,+ mimi na wewe, nalo liwe ushahidi kati yangu nawe.”+ 45 Basi Yakobo akachukua jiwe, akalisimamisha liwe nguzo.+ 46 Kisha Yakobo akawaambia ndugu zake: “Chukueni mawe!” Nao wakachukua mawe na kufanyiza rundo.+ Baada ya hayo wakala huko juu ya hilo rundo. 47 Labani akaanza kuliita Yegar-sahadutha, lakini Yakobo akaliita Galeedi.

48 Ndipo Labani akasema: “Rundo hili ni ushahidi kati yangu na wewe leo.” Hiyo ndiyo sababu akaliita jina lake Galeedi,+ 49 na Mnara wa Mlinzi, kwa sababu alisema: “Yehova na alinde kati yangu na wewe wakati tunapokuwa hatuonani.+ 50 Ukiwatesa binti zangu+ na ukichukua wake kuongezea binti zangu, hakuna mwanadamu aliye pamoja nasi. Ona! Mungu ni shahidi kati yangu na wewe.”+ 51 Na Labani akaendelea kumwambia Yakobo: “Tazama, hapa pana rundo na nguzo ndiyo hii hapa ambayo nimesimamisha kati yangu na wewe. 52 Rundo hili ni ushahidi, na hii nguzo ni kitu kinachotoa ushahidi,+ kwamba mimi sitapita rundo hili kuja juu yako na kwamba wewe hutapita rundo hili na nguzo hii kuja juu yangu kunidhuru.+ 53 Acha mungu wa Abrahamu+ na mungu wa Nahori+ ahukumu kati yetu, mungu wa baba yao.” Lakini Yakobo akaapa kwa Hofu ya baba yake Isaka.+

54 Baada ya hayo Yakobo akachinja dhabihu katika huo mlima na kuwaalika ndugu zake wale mkate.+ Basi wakala mkate na kukaa usiku huo mlimani. 55 Hata hivyo, Labani akaamka asubuhi na mapema, akawabusu+ watoto wake na binti zake, akawabariki.+ Kisha Labani akaondoka akarudi kwake.+

32 Naye Yakobo akaondoka akaenda zake, na malaika za Mungu sasa wakakutana naye.+ 2 Bila kukawia, Yakobo alipowaona akasema: “Hii ni kambi ya Mungu!”+ Kwa hiyo akapaita mahali hapo Mahanaimu.+

3 Kisha Yakobo akatuma wajumbe+ mbele yake kwenda kwa Esau ndugu yake kwenye nchi ya Seiri,+ eneo la Edomu,+ 4 naye akawaamuru, akisema: “Haya ndiyo ambayo mtamwambia bwana wangu,+ Esau, ‘Mtumishi wako Yakobo amesema hivi: “Nimekaa pamoja na Labani nikiwa mgeni kwa muda mrefu mpaka sasa.+ 5 Nami nimekuja kuwa na ng’ombe na punda, kondoo, na watumishi wanaume na wajakazi,+ nami ningependa kupeleka neno kumjulisha bwana wangu, ili nipate kibali machoni pako.”’”+

6 Baada ya muda hao wajumbe wakarudi kwa Yakobo, wakisema: “Tulifika kwa ndugu yako Esau, naye pia yuko njiani akija kukupokea, na pamoja naye wanaume mia nne.”+ 7 Naye Yakobo akaogopa sana, akaanza kuhangaika.+ Kwa hiyo akawagawanya watu waliokuwa pamoja naye kuwa kambi mbili, na makundi na ng’ombe na ngamia,+ 8 naye akasema: “Esau akija na kushambulia kambi moja, basi bila shaka kambi moja itabaki iponyoke.”+

9 Baada ya hayo Yakobo akasema: “Ee Mungu wa baba yangu Abrahamu na Mungu wa baba yangu Isaka,+ Ee Yehova, wewe unayeniambia, ‘Rudi kwenye nchi yako na kwa watu wa jamaa yako nami nitakutendea vema,’+ 10 mimi sistahili fadhili zote zenye upendo na uaminifu wote ambao umemwonyesha mtumishi wako,+ kwa maana nilivuka huu mto Yordani nikiwa na fimbo yangu tu na sasa nimekuwa kambi mbili.+ 11 Nakuomba,+ unikomboe kutoka katika mkono wa ndugu yangu, kutoka katika mkono wa Esau, kwa sababu mimi ninaogopa kwamba huenda akaja na kunishambulia,+ mama pamoja na watoto. 12 Nawe, umesema, ‘Bila shaka nitakutendea vema nami nitaufanya uzao wako uwe kama chembe za mchanga wa baharini, usioweza kuhesabika kwa sababu ya wingi wake.’”+

13 Naye akaendelea kukaa hapo usiku huo. Na kutoka katika kile kilichokuja kuwa mkononi mwake akachukua zawadi kwa ajili ya Esau ndugu yake:+ 14 mbuzi-jike 200 na mbuzi-dume 20, kondoo-jike 200 na kondoo-dume 20, 15 ngamia 20 wanaonyonyesha na watoto wao, ng’ombe 40 na ng’ombe-dume 10, punda-jike 20 na punda 10 waliokomaa.+

16 Kisha akawapa watumishi wake kundi moja moja, kundi moja baada ya lingine na kwa kurudia-rudia akawaambia watumishi wake: “Vukeni mbele yangu, nanyi mnapaswa kuweka nafasi kati ya kundi na kundi.”+ 17 Tena akamwamuru yule wa kwanza, akisema: “Ikiwa Esau ndugu yangu atakupokea na kukuuliza, akisema, ‘Wewe ni wa nani, nawe unaenda wapi na hawa walio mbele yako ni wa nani?’ 18 ndipo utasema, ‘Ni wa mtumishi wako, Yakobo. Ni zawadi,+ iliyotumwa kwa bwana wangu,+ Esau, na tazama! yeye mwenyewe yuko nyuma yetu pia.’” 19 Naye akamwamuru tena yule wa pili, na wa tatu pia, na wote wale wenye kufuata hayo makundi pia, akisema: “Kulingana na neno hili ninyi mtasema na Esau mtakapokutana naye.+ 20 Nanyi pia mnapaswa kusema, ‘Tazama, mtumishi wako Yakobo yuko nyuma yetu.’”+ Kwa maana alisema moyoni mwake: “Huenda nikamtuliza kwa zawadi inayoenda mbele yangu,+ na baadaye mimi nitaona uso wake. Labda atanipokea kwa fadhili.”+ 21 Kwa hiyo ile zawadi ikavushwa mbele yake, lakini yeye mwenyewe akakaa kambini usiku huo.+

22 Baadaye usiku huo akaondoka, akachukua wake zake+ wawili na wajakazi+ wake wawili na wanawe+ wachanga kumi na mmoja akavuka kivuko cha Yaboki.+ 23 Basi akawachukua, akawavusha bonde la mto,+ naye akavusha alivyokuwa navyo.

24 Mwishowe Yakobo akabaki peke yake. Ndipo mwanamume mmoja akaanza kupigana mweleka pamoja naye mpaka kulipopambazuka.+ 25 Yeye alipoona kwamba hakuwa amemshinda,+ akagusa tundu la fundo la paja lake; nalo tundu la fundo la paja la Yakobo likateguka wakati wa kupigana naye mweleka.+ 26 Baada ya hayo akasema; “Niache niende, kwa maana kumepambazuka.” Naye akajibu, akasema: “Mimi sitakuacha uende mpaka unibariki kwanza.”+ 27 Kwa hiyo akamwambia: “Jina lako ni nani?” akajibu, akasema: “Yakobo.” 28 Kisha akasema: “Hutaitwa tena Yakobo bali Israeli,+ kwa maana wewe umeshindana+ na Mungu na wanadamu hata ukashinda mwishowe.” 29 Naye Yakobo akauliza na kusema: “Tafadhali, niambie jina lako.” Lakini, yeye akasema: “Kwa nini unauliza jina langu?”+ Kisha akambariki huko. 30 Basi Yakobo akapaita mahali hapo Penieli,+ kwa sababu, kama alivyosema, “Mimi nimemwona Mungu uso kwa uso na bado nafsi yangu ikakombolewa.”+

31 Nalo jua likaanza kuangaza juu yake mara tu alipopita karibu na Penueli, naye alikuwa akichechemea kwenye paja lake.+ 32 Ndiyo sababu wana wa Israeli hawana desturi ya kula kano ya mshipa wa paja, ulio kwenye tundu la fundo la paja, mpaka leo hii, kwa sababu aligusa tundu la fundo la paja la Yakobo karibu na kano ya mshipa wa paja.+

33 Baada ya muda Yakobo aliinua macho yake akaona, na tazama, Esau alikuwa anakuja na pamoja naye walikuwa wanaume mia nne.+ Basi akagawanya watoto kwa Lea na kwa Raheli na kwa wale wajakazi wawili,+ 2 naye akawaweka wajakazi na watoto wao kwanza kabisa+ na Lea na watoto wake baada yao+ na Raheli na Yosefu nyuma yao.+ 3 Naye mwenyewe akapita mbele yao akaanza kuinama mpaka chini mara saba mpaka alipomkaribia ndugu yake.+

4 Kisha Esau akaanza kukimbia kwenda kumpokea.+ Naye akaanza kumkumbatia+ na kumwangukia shingoni, akambusu, nao wakatokwa na machozi. 5 Kisha akainua macho yake akaona wale wanawake na wale watoto na kusema: “Hawa walio pamoja nawe ni nani?” naye akasema: “Watoto ambao Mungu amemkubalia mtumishi wako kuwa nao.”+ 6 Ndipo wale wajakazi wakaja mbele, wao pamoja na watoto wao, wakainama chini; 7 na Lea pia akaja mbele, na watoto wake, nao wakainama chini, na baadaye Yosefu akaja mbele, na Raheli, nao wakainama chini.+

8 Ndipo yeye akasema: “Unamaanisha nini kwa kambi yote hii ya wasafiri ambao nimekutana nao?”+ Naye akajibu, akasema: “Kusudi nipate kibali machoni pa bwana wangu.”+ 9 Kisha Esau akasema: “Nina vitu vingi, ndugu yangu.+ Vilivyo vyako na viendelee kuwa vyako.” 10 Lakini Yakobo akasema: “Hapana, tafadhali. Ikiwa, sasa, nimepata kibali machoni pako,+ basi ichukue zawadi yangu mkononi mwangu, kwa sababu kwa kupatana na kusudi lake mimi nimeona uso wako kana kwamba ni kuona uso wa Mungu kwa kuwa umenipokea vizuri.+ 11 Tafadhali, ichukue zawadi ya baraka yangu iliyoletwa kwako,+ kwa sababu Mungu amenipa kibali na kwa sababu nina kila kitu.”+ Naye akaendelea kumhimiza, hata akaichukua.+

12 Baadaye Esau akasema: “Na tuondoke twende, nami niende mbele yako.” 13 Lakini akamwambia: “Bwana wangu anajua kwamba hawa watoto ni dhaifu na kondoo na ng’ombe wanaonyonyesha wako chini ya usimamizi wangu.+ Nao wakiwaendesha haraka mno kwa siku moja, basi kundi zima litakufa bila shaka.+ 14 Tafadhali, bwana wangu na apite mbele ya mtumishi wake, lakini acha mimi mwenyewe niendelee na safari kwa wakati wangu kulingana na mwendo wa mifugo+ walio mbele yangu na kulingana na mwendo wa watoto+ mpaka nimfikie bwana wangu huko Seiri.”+ 15 Kisha Esau akasema: “Tafadhali, acha niweke chini ya mamlaka yako baadhi ya watu walio pamoja nami.” Naye akajibu, akasema: “Kwa nini hivyo? Acha nipate kibali machoni pa bwana wangu.”+ 16 Basi siku hiyo Esau akageuka, akaenda zake mpaka Seiri.

17 Naye Yakobo akaondoka kuelekea Sukothi,+ naye akajijengea nyumba na kutengeneza vibanda+ kwa ajili ya mifugo yake. Ndiyo sababu aliita jina la mahali hapo Sukothi.

18 Baada ya muda Yakobo akafika jiji la Shekemu+ lililo katika nchi ya Kanaani+ akiwa salama salimini, alipokuwa akija kutoka Padan-aramu,+ naye akapiga kambi mbele ya jiji hilo. 19 Kisha akajipatia sehemu ya shamba alipopiga hema lake kutoka kwa mkono wa wana wa Hamori baba ya Shekemu, kwa vipande mia moja vya pesa.+ 20 Baada ya hayo akasimamisha hapo madhabahu, akaiita Mungu aliye Mungu wa Israeli.+

34 Sasa Dina binti ya Lea,+ ambaye alimzalia Yakobo, alizoea kwenda nje kuwaona+ binti za nchi.+ 2 Naye Shekemu mwana wa Hamori Mhivi,+ mkuu wa nchi, akamwona, kisha akamchukua, akalala naye, akamnajisi.+ 3 Nayo nafsi yake ikaanza kushikamana na Dina binti ya Yakobo, naye akampenda huyo mwanamke kijana, akawa akiongea na huyo mwanamke kijana kwa kumshawishi. 4 Mwishowe Shekemu akamwambia Hamori baba yake:+ “Nichukulie bibi huyu mchanga awe mke wangu.”+

5 Ndipo Yakobo akasikia ya kwamba alikuwa amemnajisi Dina binti yake. Nao wanawe walikuwa na mifugo yake shambani;+ naye Yakobo akakaa kimya mpaka waingie.+ 6 Baadaye Hamori, baba ya Shekemu, akamwendea Yakobo aseme naye.+ 7 Nao wana wa Yakobo wakaingia kutoka shambani mara tu waliposikia juu ya hilo; na hao wanaume wakaumia hisia zao, wakakasirika sana,+ kwa sababu alikuwa amefanya upumbavu wenye kufedhehesha juu ya Israeli kwa kulala na binti ya Yakobo,+ wakati ambapo jambo kama hilo halipasi kufanywa.+

8 Naye Hamori akasema nao, na kuwaambia: “Nafsi ya Shekemu mwanangu imeshikamana na binti yenu.+ Tafadhali, mpeni awe mke wake.+ 9 Nanyi mfanye mapatano ya ndoa pamoja nasi.+ Mtatupa sisi binti zenu, nanyi mtajichukulia binti zetu.+ 10 Nanyi mnaweza kukaa pamoja nasi, nayo nchi itakuwa wazi kwenu. Kaeni mfanye biashara humo na kufanya makao humo.”+ 11 Kisha Shekemu akamwambia baba yake na ndugu zake: “Acheni nipate kibali machoni penu, na chochote mtakachoniambia nitawapa. 12 Ongezeni sana pesa na zawadi za ndoa mnazonitoza,+ nami niko tayari kutoa kulingana na mtakavyoniambia; ila tu nipeni huyo mwanamke kijana awe mke wangu.”

13 Nao wana wa Yakobo wakamjibu Shekemu na Hamori baba yake kwa udanganyifu, kwa sababu alikuwa amemnajisi Dina dada yao.+ 14 Nao wakaendelea kuwaambia: “Sisi hatuwezi kamwe kufanya jambo la namna hiyo, kumpa mwanamume mwenye govi+ dada yetu, kwa sababu hilo ni shutuma kwetu. 15 Ni kwa sharti hili tu tunaweza kuwapa kibali, kwamba ninyi muwe kama sisi, kila mwanamume wenu atahiriwe.+ 16 Ndipo tutakapowapa ninyi binti zetu, na sisi kujichukulia binti zenu, nasi tutakaa pamoja nanyi na kuwa kundi moja la watu.+ 17 Lakini msipotusikiliza na kutahiriwa, basi tutamchukua binti yetu twende zetu.”

18 Nayo maneno yao yakaonekana kuwa mema machoni pa Hamori na machoni pa Shekemu, mwana wa Hamori.+ 19 Naye huyo kijana hakukawia kutimiza sharti hilo,+ kwa sababu alipendezwa na binti ya Yakobo na yeye alikuwa ndiye mwenye kuheshimika+ zaidi katika nyumba nzima ya baba yake.+

20 Kwa hiyo Hamori na Shekemu mwana wake wakaenda kwenye lango la jiji lao, wakaanza kuongea na wanaume wa jiji lao,+ wakisema: 21 “Wanaume hawa ni wapenda-amani kutuelekea.+ Basi acheni wakae nchini na kufanya biashara humo kwa kuwa nchi hii ni pana kabisa mbele yao.+ Sisi tunaweza kujichukulia binti zao wawe wake zetu na binti zetu tunaweza kuwapa.+ 22 Hata hivyo, wanaume hao watatupa sisi kibali chao cha kukaa pamoja nasi ili tuwe kundi moja la watu kwa sharti hili tu, kwamba kila mwanamume wetu atahiriwe sawa na wanavyotahiriwa.+ 23 Ndipo mali zao na utajiri wao na mifugo yao yote, je, hazitakuwa zetu?+ Basi na tuwape kibali chetu wapate kukaa pamoja nasi.”+ 24 Kisha wote waliokuwa wakitoka nje kupitia lango la jiji lake wakamsikiliza Hamori na Shekemu mwana wake, na wanaume wote wakatahiriwa, wale wote wanaotoka nje kupitia lango la jiji lake.

25 Lakini ikawa kwamba siku ya tatu walipokuwa wakiumwa,+ wale wana wawili wa Yakobo, Simeoni na Lawi,+ ndugu za Dina,+ wakachukua kila mmoja wao upanga wake, wakaenda bila kutazamiwa kwenye jiji hilo na kumuua kila mwanamume.+ 26 Na wakamuua Hamori na Shekemu mwana wake kwa makali ya upanga.+ Kisha wakamchukua Dina kutoka nyumbani kwa Shekemu, wakatoka nje.+ 27 Wale wana wengine wa Yakobo wakawashambulia wanaume waliotiwa majeraha ya kufisha na kulipora jiji, kwa sababu walikuwa wamemnajisi dada yao.+ 28 Makundi yao na mifugo yao na punda zao na kile kilichokuwa jijini na kile kilichokuwa shambani wakachukua.+ 29 Na riziki yao yote na watoto wao wote waliokuwa wadogo na wake zao wakawachukua mateka, hivi kwamba wakapora vyote vilivyokuwa katika nyumba hizo.+

30 Basi Yakobo akawaambia Simeoni na Lawi:+ “Mmefanya nitengwe kwa kunifanya kuwa kitu chenye kunuka kwa wakaaji wa nchi hii,+ kwa Wakanaani na Waperizi; wakati mimi ni mdogo kwa hesabu,+ nao watakusanyika pamoja juu yangu wanishambulie, nami nitaangamizwa, mimi na nyumba yangu.” 31 Nao wakajibu, wakasema: “Je, yeyote anapaswa kumtendea dada yetu kama kahaba?”+

35 Kisha Mungu akamwambia Yakobo: “Ondoka, uende Betheli, ukakae huko,+ nawe umjengee madhabahu Mungu wa kweli, aliyekutokea ulipokuwa ukimkimbia Esau ndugu yako.”+

2 Basi Yakobo akawaambia watu wa nyumba yake na wote waliokuwa pamoja naye: “Iondoleeni mbali miungu ya kigeni iliyo katikati yenu,+ nanyi mjisafishe na kubadili nguo zenu za kujitanda,+ 3 kisha tuondoke, twende Betheli. Na huko nitamjengea madhabahu Mungu wa kweli aliyenijibu siku ya taabu+ yangu kwa kuwa alikuwa pamoja nami katika njia niliyoiendea.”+ 4 Basi wakampa Yakobo miungu yote ya kigeni+ iliyokuwa mikononi mwao na vipuli vilivyokuwa masikioni mwao, naye Yakobo akavificha+ chini ya ule mti mkubwa uliokuwa karibu na Shekemu.

5 Kisha wakasafiri, nao watu wa majiji yaliyowazunguka wakamwogopa Mungu,+ kwa hiyo hawakuwafuatilia wana wa Yakobo. 6 Mwishowe Yakobo akafika Luzi,+ katika nchi ya Kanaani, yaani, Betheli, yeye na watu wote waliokuwa pamoja naye. 7 Kisha akajenga madhabahu huko. Akaanza kupaita mahali hapo El-betheli, kwa sababu Mungu wa kweli alikuwa amejifunua kwake mahali hapo alipokuwa akimkimbia ndugu yake.+ 8 Baadaye Debora+ mwanamke mlezi wa Rebeka akafa, akazikwa sehemu ya chini ya Betheli chini ya mti mkubwa sana. Basi akauita Alon-bakuthi.

9 Sasa Mungu akamtokea Yakobo tena alipokuwa akitoka Padan-aramu,+ akambariki.+ 10 Na Mungu akamwambia: “Jina lako ni Yakobo.+ Hutaendelea kuitwa Yakobo, bali utaitwa Israeli.” Naye akaanza kumwita Israeli.+ 11 Tena Mungu akamwambia: “Mimi ni Mungu Mweza-Yote.+ Zaa uongezeke. Mataifa na kutaniko la mataifa yatatoka ndani yako, na wafalme watatoka viunoni mwako.+ 12 Nayo nchi+ ambayo nimewapa Abrahamu na Isaka, nitakupa wewe, na uzao+ wako baada yako.” 13 Kisha Mungu akapanda kutoka kwake katika mahali hapo alipokuwa amesema naye.+

14 Basi Yakobo akasimamisha nguzo katika mahali alipokuwa amesema naye,+ nguzo ya mawe, naye akamimina toleo la kinywaji juu yake na kumimina mafuta juu yake.+ 15 Naye Yakobo akapaita Betheli.+

16 Kisha wakasafiri kutoka Betheli. Nao walipokuwa mbali kiasi kabla ya kufika Efrathi,+ Raheli akaanza kuzaa, na mambo yalikuwa yakimwendea vibaya alipokuwa akizaa.+ 17 Basi alipokuwa na shida wakati wa kuzaa, yule mzalishaji akamwambia: “Usiogope, kwa maana utamzaa mwana huyu pia.”+ 18 Basi nafsi+ yake ilipokuwa ikitoka (kwa sababu alikufa)+ akamwita jina lake Ben-oni; lakini baba yake akamwita Benyamini.+ 19 Kwa hiyo Raheli akafa na kuzikwa njiani kuelekea Efrathi, yaani, Bethlehemu.+ 20 Yakobo akasimamisha nguzo juu ya kaburi lake. Hiyo ndiyo nguzo ya kaburi la Raheli mpaka leo hii.+

21 Kisha Israeli akasafiri na kupiga hema lake umbali fulani ng’ambo ya mnara wa Ederi.+ 22 Pindi moja, Israeli alipokuwa akikaa+ katika nchi hiyo, Rubeni alienda akalala na Bilha suria wa baba yake, naye Israeli akapata kusikia juu ya hilo.+

Basi Yakobo alikuwa na wana kumi na wawili. 23 Wana wa Lea walikuwa Rubeni,+ mzaliwa wa kwanza wa Yakobo, na Simeoni na Lawi na Yuda na Isakari na Zabuloni. 24 Wana wa Raheli walikuwa Yosefu na Benyamini. 25 Nao wana wa Bilha, mjakazi wa Raheli, walikuwa Dani na Naftali. 26 Nao wana wa Zilpa, mjakazi wa Lea, walikuwa Gadi na Asheri. Hawa ndio wana wa Yakobo aliowazaa akiwa Padan-aramu.

27 Mwishowe Yakobo akaenda kwa Isaka baba yake huko Mamre,+ huko Kiriath-arba,+ yaani, Hebroni, ambako Abrahamu na Isaka pia walikuwa wamekaa wakiwa wageni.+ 28 Nazo siku za Isaka zikawa miaka 180.+ 29 Kisha Isaka akakata pumzi, akafa, naye akakusanywa kwa watu wake, akiwa mzee na mwenye kutosheka na siku,+ na Esau na Yakobo wanawe wakamzika.+

36 Na hii ndiyo historia ya Esau, yaani, Edomu.+

2 Esau alitwaa wake zake kutoka kwa binti za Kanaani:+ Ada+ binti ya Eloni Mhiti+ na Oholibama+ binti ya Ana, mjukuu wa Sibeoni Mhivi, 3 na Basemathi+ binti ya Ishmaeli, dada ya Nebayothi.+

4 Na Ada akamzalia Esau, Elifazi, naye Basemathi akamzaa Reueli.

5 naye Oholibama akazaa Yeushi na Yalamu na Kora.+

Hao ndio wana wa Esau ambao wake zake walimzalia katika nchi ya Kanaani. 6 Baada ya hayo Esau akachukua wake zake na wanawe na binti zake na nafsi zote za nyumba yake na mifugo yake na wanyama wake wengine wote na mali yake yote,+ aliyokuwa amekusanya katika nchi ya Kanaani, naye akaenda nchi iliyo mbali kutoka kwa Yakobo ndugu yake,+ 7 kwa sababu mali zao zilikuwa nyingi sana wasiweze kukaa pamoja na nchi ya kigeni waliyokuwa wakikaa haikuweza kuwatoshelezea mahitaji yao kwa sababu ya mifugo yao.+ 8 Basi Esau akaanza kukaa katika eneo lenye milima la Seiri.+ Esau ni Edomu.+

9 Nayo hii ndiyo historia ya Esau baba ya Edomu katika eneo lenye milima la Seiri.+

10 Haya ndiyo majina ya wana wa Esau: Elifazi mwana wa Ada, mke wa Esau; Reueli mwana wa Basemathi, mke wa Esau.+

11 Nao wana wa Elifazi walikuwa Temani,+ Omari, Sefo, Gatamu, na Kenasi.+ 12 Naye Timna+ akawa suria wa Elifazi, mwana wa Esau. Baada ya muda akamzalia Elifazi, Amaleki.+ Hao ndio wana wa Ada, mke wa Esau.

13 Hawa ndio wana wa Reueli: Nahathi na Zera, Shamma na Miza.+ Hao ndio waliokuja kuwa wana wa Basemathi,+ mke wa Esau.

14 Na hawa ndio waliokuja kuwa wana wa Oholibama binti ya Ana, mjukuu wa Sibeoni, mke wa Esau, kwa kuwa alimzalia Esau, Yeushi na Yalamu na Kora.+

15 Hawa ndio mashehe+ wa wana wa Esau: Wana wa Elifazi, mzaliwa wa kwanza wa Esau: Shehe Temani,+ shehe Omari, shehe Sefo, shehe Kenasi, 16 shehe Kora, shehe Gatamu, shehe Amaleki. Hao ndio mashehe wa Elifazi+ katika nchi ya Edomu. Hao ndio wana waliozaliwa na Ada.

17 Hawa ndio wana wa Reueli, mwana wa Esau: Shehe Nahathi, shehe Zera, shehe Shamma, shehe Miza. Hao ndio mashehe wa Reueli katika nchi ya Edomu.+ Hao ndio wana waliozaliwa na Basemathi, mke wa Esau.

18 Na mwisho hawa ndio wana wa Oholibama, mke wa Esau: Shehe Yeushi, shehe Yalamu, shehe Kora. Hao ndio mashehe wa Oholibama binti ya Ana, mke wa Esau.

19 Hao ndio wana wa Esau, na hao ndio mashehe wao. Yeye ni Edomu.+

20 Hawa ndio wana wa Seiri, yule Mhori, wakaaji wa nchi hiyo:+ Lotani na Shobali na Sibeoni na Ana+ 21 na Dishoni na Ezeri na Dishani.+ Hao ndio mashehe wa yule Mhori, wana wa Seiri, katika nchi ya Edomu.

22 Nao wana wa Lotani wakawa Hori na Hemamu; na dada ya Lotani alikuwa Timna.+

23 Nao hawa ndio wana wa Shobali: Alvani na Manahathi na Ebali, Shefo na Onamu.

24 Nao hawa ndio wana wa Sibeoni: Aya na Ana. Huyu ndiye Ana aliyepata bubujiko la maji ya moto nyikani alipokuwa akiwachunga punda wa Sibeoni baba yake.+

25 Nao hawa ndio watoto wa Ana: Dishoni na Oholibama binti ya Ana.

26 Nao hawa ndio wana wa Dishoni: Hemdani na Eshbani na Ithrani na Kerani.+

27 Hawa ndio wana wa Ezeri: Bilhani na Zaavani na Akani.

28 Hawa ndio wana wa Dishani: Usi na Arani.+

29 Hawa ndio mashehe wa yule Mhori: Shehe Lotani, shehe Shobali, shehe Sibeoni, shehe Ana, 30 shehe Dishoni, shehe Ezeri, shehe Dishani.+ Hao ndio mashehe wa yule Mhori kulingana na mashehe wao katika nchi ya Seiri.

31 Sasa hawa ndio wafalme waliotawala katika nchi ya Edomu+ kabla ya mfalme yeyote kuwatawala wana wa Israeli.+ 32 Naye Bela mwana wa Beori akatawala Edomu,+ na jina la jiji lake lilikuwa Dinhaba. 33 Na Bela alipokufa, Yobabu mwana wa Zera kutoka Bosra+ akaanza kutawala badala yake.+ 34 Yobabu alipokufa, Hushamu kutoka katika nchi ya Watemani+ akaanza kutawala badala yake.+ 35 Hushamu alipokufa, Hadadi mwana wa Bedadi, aliyewashinda Wamidiani+ katika nchi ya Moabu,+ akaanza kutawala badala yake, nalo jina la jiji lake lilikuwa Avithi.+ 36 Hadadi alipokufa, Samla kutoka Masreka akaanza kutawala badala yake.+ 37 Samla alipokufa, Shauli kutoka Rehobothi kando ya ule Mto akaanza kutawala badala yake.+ 38 Shauli alipokufa, Baal-hanani mwana wa Akbori akaanza kutawala badala yake.+ 39 Baal-hanani mwana wa Akbori alipokufa, Hadari akaanza kutawala badala yake; na jina la jiji lake lilikuwa Pau, nalo jina la mke wake lilikuwa Mehetabeli binti ya Matredi binti ya Mezahabu.+

40 Basi haya ndiyo majina ya mashehe wa Esau kulingana na familia zao, kulingana na mahali pao, kwa majina yao: Shehe Timna, shehe Alva, shehe Yethethi,+ 41 shehe Oholibama, shehe Ela, shehe Pinoni,+ 42 shehe Kenasi, shehe Temani, shehe Mibsari,+ 43 shehe Magdieli, shehe Iramu. Hao ndio mashehe wa Edomu+ kulingana na makao yao katika nchi yao.+ Huyu ndiye Esau baba ya Edomu.+

37 Naye Yakobo akaendelea kukaa katika nchi ya kigeni ya baba yake,+ katika nchi ya Kanaani.+

2 Hii ndiyo historia ya Yakobo.

Yosefu,+ alipokuwa na umri wa miaka kumi na saba, alikuwa akichunga kondoo pamoja na ndugu zake kati ya kundi,+ na, kwa kuwa alikuwa mvulana tu, alikuwa pamoja na wana wa Bilha+ na wana wa Zilpa,+ wake za baba yake. Basi Yosefu akamletea baba yake habari mbaya juu yao.+ 3 Naye Israeli alimpenda Yosefu kuliko wanawe wengine wote,+ kwa sababu alikuwa mwana wa uzee wake; naye alikuwa amemshonea vazi refu lenye mistari linalofanana na shati.+ 4 Ndugu zake walipoona kwamba baba yao alimpenda kuliko ndugu zake wote, wakaanza kumchukia,+ nao hawakusema naye kwa amani.+

5 Baada ya muda Yosefu aliota ndoto, akawasimulia ndugu zake,+ nao wakawa na sababu zaidi ya kumchukia. 6 Aliwaambia hivi: “Tafadhali, sikilizeni ndoto hii ambayo nimeota.+ 7 Tazama, tulikuwa tukifunga miganda katikati ya shamba wakati ambapo tazama, mganda wangu uliinuka, ukasimama wima nayo miganda yenu ikauzunguka na kuuinamia mganda wangu.”+ 8 Nao ndugu zake wakamwambia: “Je, kwa kweli utakuwa mfalme juu yetu?+ Au utatutawala?”+ Basi wakapata sababu mpya ya kumchukia kwa sababu ya ndoto zake na maneno yake.

9 Baadaye akaota ndoto nyingine tena, akawasimulia ndugu zake na kusema: “Tazama nimeota ndoto tena, na tazama, jua na mwezi na nyota kumi na moja zilikuwa zikiniinamia.”+ 10 Kisha akamsimulia baba yake na ndugu zake vilevile, na baba yake akamkemea na kumwambia:+ “Ndoto hii ambayo umeota inamaanisha nini? Je, mimi na pia mama yako na ndugu zako kwa kweli tutakuja na kukuinamia?” 11 Na ndugu zake wakaanza kumwonea wivu,+ lakini baba yake akayatia moyoni maneno hayo.+

12 Sasa ndugu zake wakaenda kulisha kundi la baba yao karibu na Shekemu.+ 13 Baada ya muda, Israeli akamwambia Yosefu: “Je, ndugu zako hawachungi makundi karibu na Shekemu? Njoo, nikutume kwao.” Basi akamjibu, akamwambia: “Mimi hapa!”+ 14 Basi akamwambia: “Tafadhali, nenda. Kaone kama ndugu zako wako salama salimini na kama kundi liko salama salimini, halafu uniletee habari.”+ Basi akamtuma toka nchi tambarare ya chini ya Hebroni,+ naye akaenda kuelekea Shekemu. 15 Baadaye mwanamume fulani akamkuta na tazama, alikuwa akizunguka-zunguka shambani. Basi mwanamume huyo akamuuliza: “Unatafuta nini?” 16 Akajibu: “Nawatafuta ndugu zangu. Tafadhali, niambie, Wanachunga makundi wapi?” 17 Naye mwanamume huyo akamwambia: “Wameondoka hapa, kwa sababu niliwasikia wakisema, ‘Twendeni Dothani.’” Kwa hiyo akaendelea kuwafuata ndugu zake, akawapata huko Dothani.

18 Ndugu zake wakamwona akiwa mbali, na kabla hajakaribia wakaanza kumpangia kwa ujanja hila ya kumuua.+ 19 Basi wakasemezana: “Tazama! Yule mwota-ndoto anakuja.+ 20 Basi na tumuue, tumtupe ndani ya moja la mashimo ya maji;+ halafu tutasema mnyama mkali wa mwitu alimrarua.+ Ndipo tuone itakuwaje kwa ndoto zake.” 21 Rubeni aliposikia hilo alijaribu kumwokoa kutoka mikononi mwao.+ Kwa hiyo akasema: “Tusiipige nafsi yake kiasi cha kuiua.”+ 22 Naye Rubeni akaendelea kuwaambia: “Msimwage damu.+ Mtupeni ndani ya shimo hili la maji lililo nyikani wala msimtendee kwa jeuri.”+ Alikusudia kumwokoa kutoka katika mikono yao ili amrudishe kwa baba yake.

23 Basi mara tu Yosefu alipowafikia ndugu zake, wakamvua Yosefu vazi lake refu, naam, lile vazi refu lenye mistari alilokuwa amevaa;+ 24 kisha wakamchukua na kumtupa ndani ya hilo shimo la maji.+ Wakati huo shimo hilo lilikuwa tupu; halikuwa na maji ndani yake.

25 Kisha wakaketi ili kula mkate.+ Walipoinua macho yao na kutazama, kumbe, kulikuwa na msafara wa Waishmaeli+ uliokuwa ukija kutoka Gileadi, na ngamia zao walikuwa wamebeba ubani mweusi na zeri na gome lenye utomvu,+ wakiwa njiani kuzipeleka Misri. 26 Basi Yuda akawaambia ndugu zake: “Kungekuwa faida gani tukimuua ndugu yetu na kufunika damu yake?+ 27 Njooni, na tumuuze kwa Waishmaeli,+ nasi tusiinue mkono wetu juu yake.+ Bado yeye ni ndugu yetu, nyama yetu.” Kwa hiyo wakamsikiliza ndugu yao.+ 28 Wanaume, wanabiashara Wamidiani,+ wakapitia hapo. Basi wakamvuta na kumpandisha Yosefu kutoka katika lile shimo la maji+ kisha wakamuuza kwa wale Waishmaeli kwa vipande 20 vya fedha.+ Mwishowe wanabiashara hao wakampeleka Yosefu Misri.

29 Baadaye Rubeni akarudi kwenye lile shimo la maji na tazama Yosefu hakuwemo. Basi akayararua mavazi yake.+ 30 Aliporudi kwa wale ndugu zake wengine akasema: “Mtoto hayuko! Na mimi—mimi kwa kweli nitaenda wapi?”+

31 Hata hivyo, wakalichukua lile vazi refu la Yosefu, wakamchinja mbuzi-dume na kulichovya-chovya vazi hilo katika damu.+ 32 Kisha wakalipeleka lile vazi refu lenye mistari kwa baba yao na kusema: “Hiki ndicho tulichopata. Tafadhali, chunguza+ kama ni lile vazi refu la mwana wako au hapana.”+ 33 Naye akalichunguza na kusema: “Ni vazi la mwanangu! Mnyama-mwitu mkali amemrarua!+ Hakika Yosefu ameraruliwa vipande-vipande!”+ 34 Basi Yakobo akararua nguo zake za kujitanda, akavaa nguo za magunia viunoni mwake, akamwombolezea mwana wake siku nyingi.+ 35 Nao wanawe wote na binti zake wote wakawa wakiondoka ili kumfariji,+ lakini akawa akizidi kukataa kufarijiwa na kusema:+ “Kwa maana nitashuka kuingia katika Kaburi* nikimwombolezea mwanangu!” Na baba yake akaendelea kumlilia.

36 Hata hivyo, Wamidiani wakamuuza Misri kwa Potifa, ofisa wa makao ya Farao,+ mkuu wa walinzi.+

38 Sasa ikawa wakati huo kwamba Yuda aliposhuka kutoka kwa ndugu zake, alipiga hema karibu na mwanamume, Mwadulamu,+ na jina lake lilikuwa Hira. 2 Na huko Yuda akamwona binti ya Mkanaani+ fulani aliyekuwa akiitwa Shua. Basi akamchukua, akalala naye. 3 Naye akapata mimba. Baadaye akazaa mwana, akamwita jina lake Eri.+ 4 Akapata mimba tena. Akazaa mwana, akamwita jina lake Onani. 5 Tena akazaa mwana, akamwita jina lake Shela. Alipomzaa, Yuda alikuwa Akzibu.+

6 Baada ya muda Yuda akamchukulia Eri mzaliwa wake wa kwanza mke. Na mke huyo aliitwa Tamari.+ 7 Lakini Eri, mzaliwa wa kwanza wa Yuda, alikuwa mbaya machoni pa Yehova;+ kwa hiyo Yehova akamuua.+ 8 Basi Yuda akamwambia Onani: “Lala na mke wa ndugu yako, ufanye ndoa ya ndugu-mkwe pamoja naye umwinulie uzao ndugu yako.”+ 9 Lakini Onani alijua kwamba uzao huo haungekuwa wake;+ basi alipolala na mke wa ndugu yake akamwaga chini shahawa zake ili asimpe ndugu yake uzao.+ 10 Sasa jambo alilofanya lilikuwa baya machoni pa Yehova;+ kwa hiyo akamuua yeye pia.+ 11 Basi Yuda akamwambia Tamari binti-mkwe wake: “Kaa ukiwa mjane katika nyumba ya baba yako mpaka Shela mwanangu akue.”+ Kwa maana alisema moyoni mwake: “Huenda yeye pia akafa kama ndugu zake.”+ Basi Tamari akaenda, naye akaendelea kukaa katika nyumba ya baba yake.+

12 Basi siku zikawa nyingi naye binti ya Shua, mke wa Yuda,+ akafa; naye Yuda akashika kile kipindi cha kuomboleza.+ Kisha akaenda kwa wanyoaji wa kondoo zake huko Timna,+ yeye na mwenzake, Hira, Mwadulamu.+ 13 Ndipo Tamari akaambiwa: “Tazama baba-mkwe wako anaenda Timna kuwanyoa kondoo zake.”+ 14 Basi akayavua mavazi ya ujane wake, akavaa shali na kujifunika uso, naye akaketi chini kwenye mwingilio wa Enaimu, jiji lililo katika barabara inayokwenda Timna. Kwa maana aliona ya kwamba Shela alikuwa ameshakuwa mtu mzima na bado hakuwa amekabidhiwa kwake awe mke wake.+

15 Mara Yuda alipomwona, akamfikiria kuwa ni kahaba,+ kwa sababu alikuwa ameufunika uso wake.+ 16 Basi akamwendea kando ya barabara akamwambia: “Tafadhali, niruhusu nilale nawe.”+ Kwa kuwa hakujua kwamba alikuwa binti-mkwe wake.+ Hata hivyo, akasema: “Utanipa nini ili ulale nami?”+ 17 Akasema: “Mimi mwenyewe nitakuletea mwana-mbuzi kutoka katika kundi.” Lakini akasema: “Je, utatoa rehani mpaka utakapomleta?”+ 18 Naye akasema: “Ni rehani gani nitakayokupa?” akasema: “Pete yako ya muhuri+ na kamba yako na fimbo yako iliyo mkononi mwako.” Basi akampa vitu hivyo, akalala naye, naye akapata mimba. 19 Kisha akaondoka, akaenda, akaivua ile shali na kuvaa mavazi ya ujane wake.+

20 Na Yuda akamtuma mwenzake Mwadulamu+ ampeleke mwana-mbuzi ili arudishiwe rehani kutoka mkononi mwa yule mwanamke, lakini hakumpata kamwe. 21 Akawauliza-uliza watu wa mahali pake, akisema: “Yuko wapi yule kahaba wa hekaluni katika Enaimu kando ya barabara?” Lakini wakawa wakisema: “Hakujawahi kuwa na kahaba wa hekaluni+ mahali hapa.” 22 Mwishowe akarudi kwa Yuda na kumwambia: “Sikumpata kamwe, tena, watu wa mahali hapo walisema, ‘Hakujawahi kuwa na kahaba wa hekaluni mahali hapa.’” 23 Basi Yuda akasema: “Mwache avichukue viwe vyake, tusije tukadharaulika.+ Tena, nimemtumia mwana-mbuzi huyu, lakini wewe hukumpata kamwe.”

24 Hata hivyo, miezi mitatu hivi baadaye Yuda akaambiwa: “Tamari binti-mkwe wako amefanya ukahaba,+ na tazama ana mimba+ pia kutokana na ukahaba wake.” Ndipo Yuda akasema: “Mtoeni nje ateketezwe.”+ 25 Alipokuwa akitolewa nje, akapeleka ujumbe kwa baba-mkwe wake, akisema: “Nina mimba ya mwanamume mwenye vitu hivi.”+ Naye akaongezea: “Tafadhali, vichunguze+ ni vya nani, pete ya muhuri na kamba na fimbo.”+ 26 Basi Yuda akavichunguza na kusema:+ “Yeye ni mwadilifu kuliko mimi,+ kwa sababu sikumpa Shela mwanangu awe mke wake.”+ Naye hakulala naye tena baada ya hayo.+

27 Sasa ilitukia kwamba wakati wake wa kuzaa ulipofika, tazama, kulikuwa na mapacha tumboni mwake. 28 Tena, alipokuwa akizaa mmoja akaunyoosha mkono wake, na mara moja mzalishaji akamfunga kitambaa chekundu mkononi, akisema: “Huyu alitoka kwanza.” 29 Mwishowe ikatokea kwamba mara tu alipourudisha mkono wake, tazama ndugu yake akatoka. Mzalishaji akasema: “Unamaanisha nini kwa hili, kwamba umejipasulia msamba?” Basi akaitwa jina lake Perezi.+ 30 Na baadaye ndugu yake ambaye mkono wake ulifungwa kitambaa chekundu akatoka naye jina lake akaitwa Zera.+

39 Basi Yosefu akapelekwa Misri,+ na Potifa,+ ofisa wa makao ya Farao, mkuu wa walinzi, Mmisri, akamnunua kutoka kwa Waishmaeli+ waliokuwa wamemleta huko. 2 Lakini Yehova alikuwa pamoja na Yosefu hata akafanikiwa,+ akaja kusimamia nyumba ya bwana wake, yule Mmisri. 3 Naye bwana wake akaona kwamba Yehova alikuwa pamoja naye na kwamba kila jambo alilokuwa akifanya Yehova alikuwa akilifanikisha mikononi mwake.

4 Na Yosefu akazidi kupata kibali machoni pake naye akamtumikia siku zote hata akamweka juu ya nyumba yake,+ na vitu vyote vilivyokuwa vyake akaviweka mkononi mwake. 5 Ikawa kwamba tangu alipomweka asimamie nyumba yake na vyote vilivyokuwa vyake, Yehova akazidi kuibariki nyumba ya Mmisri huyo kwa sababu ya Yosefu, na Yehova akabariki vitu vyote alivyokuwa navyo nyumbani na shambani.+ 6 Mwishowe akaweka katika mkono wa Yosefu vitu vyake vyote,+ wala hakujua kilichokuwa chake ila mkate aliokuwa akila. Pia, Yosefu akakua akawa mwenye umbo zuri na mwenye sura ya kupendeza.

7 Sasa baada ya mambo hayo ikawa kwamba mke wa bwana wake akaanza kuinua macho+ yake kumwelekea Yosefu na kusema: “Lala nami.”+ 8 Lakini akawa akikataa,+ naye alikuwa akimwambia mke wa bwana wake: “Tazama bwana wangu hajui kilicho nami nyumbani, na vyote ameviweka mkononi mwangu.+ 9 Hakuna yeyote aliye mkubwa zaidi yangu katika nyumba hii, naye hakunizuilia chochote ila wewe, kwa sababu wewe ni mke wake.+ Basi ninawezaje kufanya ubaya huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?”+

10 Basi ikawa kwamba aliposema na Yosefu siku baada ya siku, hakumsikiliza kamwe alale kando yake, awe pamoja naye.+ 11 Lakini ikawa kwamba siku hiyo sawa na siku nyinginezo akaingia nyumbani afanye kazi zake, na hapakuwa na yeyote kati ya watu wa nyumba aliyekuwa ndani ya nyumba hiyo.+ 12 Basi mwanamke huyo akamshika kwa vazi lake,+ akisema: “Lala nami!”+ Lakini akaliacha vazi lake mkononi mwake, akakimbia na kwenda nje.+ 13 Basi mara huyo mwanamke alipoona ya kuwa ameliacha vazi lake mkononi mwake ili aweze kukimbia nje, 14 akaanza kuwaita watu wa nyumba yake kwa sauti kubwa na kuwaambia: “Tazameni! Alituletea mtu, Mwebrania, atufanyie dhihaka. Alinijia ili alale nami, lakini nikalia kwa sauti kubwa.+ 15 Na mara tu aliposikia nimepaaza sauti na kuanza kulia, akaliacha vazi lake kando yangu, akakimbia nje.” 16 Baada ya hayo akaliweka vazi lake kando yake mpaka bwana wake aliporudi nyumbani kwake.+

17 Kisha akamwambia maneno hayo, akisema: “Yule mtumishi Mwebrania uliyetuletea alinijia ili anidhihaki. 18 Lakini mara tu nilipopaaza sauti na kulia, akaliacha vazi lake kando yangu, akakimbia nje.”+ 19 Ikatokea kwamba mara tu bwana wake aliposikia maneno ya mke wake, akisema: “Mtumishi wako alinifanyia hivi na hivi,” hasira yake ikawaka.+ 20 Basi bwana wa Yosefu akamchukua akamtia katika nyumba ya gereza, mahali ambapo wafungwa wa mfalme waliwekwa kizuizini, naye akaendelea kuwa humo katika nyumba ya gereza.+

21 Hata hivyo, Yehova akaendelea kuwa pamoja na Yosefu, akazidi kumfanyia fadhili zenye upendo na kumwezesha kupata kibali machoni pa ofisa mkuu wa nyumba ya gereza.+ 22 Ofisa mkuu wa nyumba ya gereza akawatia mkononi mwa Yosefu wafungwa wote waliokuwa katika nyumba hiyo ya gereza; na yote waliyokuwa wakifanya humo yeye ndiye aliyekuwa akiagiza yafanywe.+ 23 Yule ofisa mkuu wa nyumba ya gereza hakuwa akiangalia kitu chochote kilichokuwa mkononi mwake, kwa sababu Yehova alikuwa pamoja na Yosefu na yale aliyokuwa akifanya Yehova aliyafanikisha.+

40 Sasa ikawa kwamba baada ya mambo hayo, mnyweshaji+ wa mfalme wa Misri na mwokaji walimtendea dhambi bwana wao, mfalme wa Misri.+ 2 Farao akakasirishwa na hao watumishi wake wawili,+ mkuu wa wanyweshaji na mkuu wa waokaji.+ 3 Basi akawatia katika jela ya nyumba ya mkuu wa walinzi,+ katika ile nyumba ya gereza,+ mahali ambapo Yosefu alikuwa mfungwa. 4 Kisha mkuu wa walinzi akampa Yosefu mgawo awe nao ili awahudumie;+ nao wakakaa jela siku kadhaa.

5 Na wote wawili wakaota ndoto,+ kila mmoja ndoto yake katika huo usiku mmoja,+ kila mmoja ndoto yake yenye tafsiri yake,+ mnyweshaji na mwokaji wa mfalme wa Misri waliokuwa wafungwa katika nyumba ya gereza.+ 6 Yosefu alipowajia asubuhi na kuwaona, tazama, walionekana wana huzuni.+ 7 Naye akawauliza hao maofisa wa Farao waliokuwa naye katika jela ya nyumba ya bwana wake, akisema: “Kwa nini nyuso zenu zina huzuni leo?”+ 8 Wakamjibu: “Tumeota ndoto, wala hatuna mtafsiri.” Basi Yosefu akawaambia: “Je, tafsiri si za Mungu?+ Tafadhali, nisimulieni.”

9 Naye mkuu wa wanyweshaji akamsimulia Yosefu ndoto yake akisema: “Katika ndoto yangu, kulikuwako mzabibu mbele yangu. 10 Na kwenye mzabibu kulikuwako matawi matatu, na ulionekana unaota machipukizi.+ Ukachanua maua. Vishada vyake vikaivisha zabibu zake. 11 Kikombe cha Farao kilikuwa mkononi mwangu, nami nikachukua zabibu na kuziminya ndani ya kikombe cha Farao.+ Halafu nikakiweka kikombe mkononi mwa Farao.”+ 12 Kisha Yosefu akamwambia: “Hii ndiyo tafsiri yake.+ Yale matawi matatu ni siku tatu. 13 Baada ya siku tatu Farao atakiinua kichwa chako naye atakurudisha katika cheo chako;+ nawe bila shaka utampa Farao kikombe mkononi mwake, kulingana na desturi ya zamani ulipokuwa mnyweshaji wake.+ 14 Hata hivyo, unikumbuke mara tu mambo yatakapokuendea vema,+ tafadhali, usikose kunitendea fadhili zenye upendo na kunitaja kwa Farao,+ nawe unitoe nje ya nyumba hii. 15 Kwa maana kwa kweli nilitekwa nyara kutoka katika nchi ya Waebrania;+ na hapa pia sijafanya jambo lolote kamwe hata wanitie katika tundu hili la gereza.”+

16 Mkuu wa waokaji alipoona kwamba Yosefu ametafsiri jambo jema, yeye naye akamwambia Yosefu: “Mimi pia nilikuwa katika ndoto yangu, na tazama, vikapu vitatu vya mkate mweupe vilikuwa kichwani pangu. 17 Ndani ya kikapu cha juu kabisa mlikuwemo namna zote za vyakula vya Farao,+ vitu vya mwokaji, pia kulikuwako ndege+ wakizila katika kikapu juu ya kichwa changu.” 18 Kisha Yosefu akajibu na kusema: “Hii ndiyo tafsiri yake:+ Vile vikapu vitatu ni siku tatu. 19 Baada ya siku tatu tokea sasa Farao atakiinua kichwa chako na kukiondoa juu yako naye atakutundika juu ya mti;+ nao ndege wataila nyama yako.”+

20 Basi siku ya tatu ilikuwa sikukuu ya kuzaliwa kwa Farao,+ naye akawafanyia karamu watumishi wake wote na kukiinua kichwa cha mkuu wa wanyweshaji na kichwa cha mkuu wa waokaji katikati ya watumishi wake.+ 21 Akamrudisha mkuu wa wanyweshaji kwenye cheo chake cha kunywesha,+ naye akaendelea kumpa Farao kikombe mkononi mwake. 22 Lakini akamtundika mkuu wa waokaji,+ kama vile Yosefu alivyokuwa amewatafsiria.+ 23 Hata hivyo, mkuu wa wanyweshaji hakumkumbuka Yosefu, naye akaendelea kumsahau.+

41 Ikawa kwamba mwishoni mwa miaka miwili kamili Farao akaota ndoto,+ na tazama, alikuwa amesimama kando ya mto Nile. 2 Na tazama, ng’ombe saba, wenye sura nzuri, wanono, wakatoka ndani ya mto Nile, nao wakaanza kula majani ya mto Nile.+ 3 Na tazama, baada yao ng’ombe wengine saba wakatoka ndani ya mto Nile, wenye sura mbaya, waliokonda,+ nao wakasimama kando ya wale ng’ombe waliokuwa ukingoni mwa mto Nile. 4 Kisha wale ng’ombe waliokuwa na sura mbaya, waliokonda, wakaanza kuwala wale ng’ombe saba waliokuwa na sura nzuri, wanono.+ Basi Farao akaamka.+

5 Hata hivyo, akarudi kulala usingizi na kuota ndoto mara ya pili. Na tazama, kulikuwa na masuke saba ya nafaka yakitokeza kwenye tawi moja, makubwa na mazuri.+ 6 Na tazama, kulikuwa na masuke saba ya nafaka, membamba, yaliyounguzwa na upepo wa mashariki,+ yakikua baada ya yale mengine.+ 7 Nayo yale masuke membamba ya nafaka yakaanza kuyameza yale masuke saba ya nafaka, makubwa, yaliyojaa.+ Basi Farao akaamka na tazama ilikuwa ni ndoto tu.

8 Ikawa kwamba asubuhi, roho yake ikafadhaika.+ Basi akawaita makuhani wote wenye kufanya uchawi wa Misri+ na watu wake wote wenye hekima,+ naye Farao akawasimulia ndoto zake.+ Lakini hakukuwa na yeyote aliyeweza kumtafsiria Farao ndoto hizo.

9 Kisha mkuu wa wanyweshaji akaongea na Farao,+ na kusema: “Dhambi zangu ninazitaja leo.+ 10 Farao aliwakasirikia watumishi wake.+ Kwa hiyo akanitia katika jela ya nyumba ya mkuu wa walinzi,+ mimi na mkuu wa waokaji. 11 Kisha sote wawili tukaota ndoto usiku mmoja, mimi na yeye. Tuliota kila mmoja ndoto yake yenye tafsiri yake.+ 12 Na kijana mmoja alikuwa humo pamoja nasi, Mwebrania,+ mtumishi wa mkuu wa walinzi.+ Tulipomsimulia,+ akatutafsiria ndoto zetu. Akamtafsiria kila mmoja kama ilivyokuwa ndoto yake. 13 Ikawa kwamba kama vile alivyotutafsiria, ndivyo ilivyotukia. Mimi akanirudisha katika cheo changu,+ lakini yeye akamtundika.”+

14 Na Farao akatuma watu wamwite Yosefu,+ kwamba wamlete upesi kutoka katika tundu la gereza.+ Basi akajinyoa+ na kubadili nguo zake za kujitanda,+ akaingia ndani kwa Farao. 15 Kisha Farao akamwambia Yosefu: “Nimeota ndoto, lakini hapana mtu wa kuitafsiri. Sasa mimi mwenyewe nimesikia ikisemwa juu yako ya kwamba unaweza kusikia ndoto na kuitafsiri.”+ 16 Ndipo Yosefu akamjibu Farao, akisema: “Mimi sipaswi kufikiriwa! Mungu atamtangazia Farao hali njema.”+

17 Naye Farao akamwambia Yosefu: “Katika ndoto yangu tazama nilikuwa nimesimama ukingoni mwa mto Nile. 18 Na tazama, ng’ombe saba wanono, wenye umbo zuri wakatoka ndani ya mto Nile, nao wakaanza kula majani ya mto Nile.+ 19 Na tazama, ng’ombe wengine saba wakatoka baada yao, dhaifu na wenye umbo baya sana, waliokonda.+ Sijapata kuwaona wabaya kama hao katika nchi yote ya Misri. 20 Na wale ng’ombe waliokonda, wabaya, wakaanza kuwala wale ng’ombe saba wanono wa kwanza.+ 21 Basi hao wakaingia matumboni mwao, na bado haingeweza kujulikana kwamba walikuwa wameingia matumboni mwao, kwa kuwa sura zao zilikuwa mbaya kama vile mwanzoni.+ Ndipo nilipoamka.

22 “Kisha nikaona katika ndoto yangu na tazama, kulikuwa na masuke saba ya nafaka yakitokeza kwenye tawi moja, yaliyojaa na mazuri.+ 23 Na tazama, kulikuwa na masuke saba ya nafaka yaliyokauka, membamba, yaliyounguzwa na upepo wa mashariki,+ yakikua baada yake. 24 Na yale masuke membamba ya nafaka yakaanza kuyameza yale masuke saba ya nafaka yaliyo mazuri.+ Basi nikawasimulia makuhani wenye kufanya uchawi,+ lakini hakuwako yeyote aliyeniambia.”+

25 Kisha Yosefu akamwambia Farao: “Ndoto ya Farao ni moja. Anayofanya Mungu wa kweli amemwambia Farao.+ 26 Wale ng’ombe saba wazuri ni miaka saba. Hali kadhalika yale masuke saba ya nafaka yaliyo mazuri ni miaka saba. Ndoto ni moja. 27 Nao wale ng’ombe saba waliokonda ambao walipanda baada yao ni miaka saba; na yale masuke saba ya nafaka yaliyo matupu, yaliyounguzwa na upepo wa mashariki,+ yatakuwa miaka saba ya njaa.+ 28 Hilo ndilo jambo ambalo nimemwambia Farao: Anayofanya Mungu wa kweli amemwezesha Farao kuona.+

29 “Tazama kuna miaka saba inayokuja ya shibe katika nchi yote ya Misri. 30 Lakini miaka saba ya njaa itakuja baada yake, nayo shibe yote ya nchi ya Misri itasahaulika nayo njaa itaimaliza nchi.+ 31 Na shibe iliyokuwako wakati mmoja katika nchi haitajulikana kwa sababu ya njaa itakayofuata, kwa kuwa itakuwa kali sana. 32 Na kwa kuwa ndoto hiyo ilirudiwa mara mbili kwa Farao inamaanisha kwamba jambo hilo limewekwa imara na Mungu wa kweli,+ na Mungu wa kweli anaharakisha kulifanya.+

33 “Basi sasa Farao na atafute mtu mwenye busara na mwenye hekima, amweke juu ya nchi ya Misri.+ 34 Farao na achukue hatua na kuwaweka waangalizi juu ya nchi,+ naye achukue sehemu moja ya tano ya nchi ya Misri wakati wa ile miaka saba ya shibe.+ 35 Nao wakusanye vyakula vyote vya miaka hiyo mizuri inayokuja, nao warundike nafaka chini ya mkono wa Farao zikiwa vyakula majijini,+ nao waviweke akiba. 36 Navyo vyakula hivyo viwe akiba ya nchi kwa ajili ya ile miaka saba ya njaa, itakayotokea katika nchi ya Misri,+ ili hii nchi isije ikafutiliwa mbali na hiyo njaa.”+

37 Basi jambo hilo likawa jema machoni pa Farao na watumishi wake wote.+ 38 Kwa hiyo Farao akawaambia watumishi wake: “Je, kwaweza kupatikana mtu mwingine kama huyu ambaye roho ya Mungu imo ndani yake?”+ 39 Kisha Farao akamwambia Yosefu: “Kwa kuwa Mungu amekuwezesha kuyajua yote hayo,+ hakuna mtu mwenye busara na mwenye hekima kama wewe.+ 40 Wewe binafsi utaisimamia nyumba yangu,+ na watu wangu wote watakutii kabisa.+ Mimi nitakuwa mkuu kuliko wewe katika kiti cha ufalme tu.”+ 41 Tena Farao akamwambia Yosefu: “Ona, nakuweka juu ya nchi yote ya Misri.”+ 42 Kisha Farao akaivua pete yake rasmi ya muhuri+ kutoka mkononi mwake, akaiweka mkononi mwa Yosefu na kumvalisha mavazi ya kitani bora, naye akaweka mkufu wa dhahabu shingoni mwake.+ 43 Tena akampandisha katika gari la pili la heshima alilokuwa nalo,+ hata wapaaze sauti mbele yake, “Avrekh!” hivyo akamweka juu ya kila kitu katika nchi ya Misri.

44 Tena Farao akamwambia Yosefu: “Mimi ni Farao, lakini bila ruhusa yako mtu yeyote asiinue mkono wake wala mguu wake katika nchi yote ya Misri.”+ 45 Kisha Farao akaliita jina la Yosefu Zafenath-panea, naye akampa Asenathi,+ binti ya Potifera kuhani wa Oni,+ awe mke wake. Naye Yosefu akaanza kwenda kotekote katika nchi ya Misri.+ 46 Naye Yosefu alikuwa na umri wa miaka 30+ aliposimama mbele ya Farao mfalme wa Misri.

Kisha Yosefu akatoka mbele ya Farao, akatembea kotekote katika nchi yote ya Misri. 47 Na wakati wa ile miaka saba ya shibe nchi ikaendelea kuzaa kwa wingi.+ 48 Naye akakusanya vyakula vyote vya ile miaka saba iliyoijia nchi ya Misri, akaviweka vyakula hivyo majijini.+ Vyakula vya shamba lililolizunguka jiji akaviweka katikati yake.+ 49 Na Yosefu akaendelea kurundika nafaka nyingi sana,+ kama mchanga wa baharini, mpaka mwishowe wakaacha kuihesabu, kwa sababu haikuwa na hesabu.+

50 Na kabla ya ule mwaka wa njaa kufika, Yosefu akazaa wana wawili,+ ambao Asenathi, binti ya Potifera kuhani wa Oni, alimzalia. 51 Basi Yosefu akamwita jina lake mzaliwa wa kwanza Manase,+ kwa sababu, kama alivyosema, “Mungu amenifanya nisahau taabu yangu yote na nyumba yote ya baba yangu.”+ 52 Naye yule wa pili akamwita jina lake Efraimu,+ kwa sababu, kama alivyosema, “Mungu ameniwezesha kuwa na uzao katika nchi ya taabu yangu.”+

53 Mwishowe miaka saba ya shibe katika nchi ya Misri ikaisha,+ 54 nayo miaka saba ya njaa ikaanza kuja, kama vile tu Yosefu alivyokuwa amesema.+ Nayo njaa ikawa katika nchi zote, lakini mkate ulipatikana katika nchi yote ya Misri.+ 55 Mwishowe nchi yote ya Misri ikawa na njaa, nao watu wakaanza kumlilia Farao awape mkate.+ Kisha Farao akawaambia Wamisri wote: “Nendeni kwa Yosefu. Lolote atakalowaambia, fanyeni.”+ 56 Na hiyo njaa ikawa juu ya uso wote wa dunia.+ Ndipo Yosefu akaanza kuyafungua maghala yote ya nafaka yaliyokuwa kati yao na kuwauzia Wamisri,+ ile njaa ilipozidi kuibana nchi ya Misri. 57 Tena, watu wa dunia yote wakaja Misri ili wanunue kutoka kwa Yosefu, kwa sababu hiyo njaa ilikuwa imeibana dunia yote.+

42 Mwishowe Yakobo akaona kwamba kuna nafaka Misri.+ Kisha akawauliza wanawe: “Kwa nini mnaendelea kutazamana?” 2 Tena akawaambia: “Tazama nimesikia kwamba kuna nafaka Misri.+ Shukeni huko mkatununulie nafaka, tupate kuendelea kuishi ili tusife.” 3 Basi ndugu+ kumi za Yosefu wakashuka waende kununua nafaka Misri. 4 Lakini Yakobo hakumruhusu Benyamini,+ ndugu ya Yosefu, aende pamoja na wale ndugu zake wengine, kwa sababu alisema: “Ili tukio lenye kufisha lisimpate.”+

5 Kwa hiyo wana wa Israeli wakafuatana na wengine waliokuwa wakienda kununua, kwa sababu kulikuwa na njaa katika nchi ya Kanaani.+ 6 Na Yosefu ndiye aliyekuwa mwenye mamlaka juu ya nchi hiyo.+ Ndiye aliyewauzia watu wote wa dunia.+ Basi ndugu za Yosefu wakaja na kumwinamia kifudifudi.+ 7 Yosefu alipowaona ndugu zake, akawatambua mara moja, lakini akajifanya asitambulike kwao.+ Basi, akaongea nao kwa ukali na kusema: “Mmetoka wapi?” nao wakajibu: “Tumetoka nchi ya Kanaani ili kununua vyakula.”+

8 Hivyo Yosefu akawatambua ndugu zake, lakini wao hawakumtambua. 9 Papo hapo Yosefu akakumbuka ndoto alizokuwa ameota juu yao,+ naye akaendelea kuwaambia: “Ninyi ni wapelelezi! Mmekuja kuona hali ya ukosefu wa ulinzi wa nchi hii!”+ 10 Kisha wakamwambia: “Sivyo, bwana wangu,+ bali watumishi wako+ wamekuja kununua vyakula. 11 Sisi sote ni wana wa mtu mmoja tu. Sisi ni watu wanyoofu. Watumishi wako si wapelelezi.”+ 12 Lakini akawaambia: “Sivyo! Kwa sababu ninyi mmekuja kuona hali ya ukosefu wa ulinzi wa hii nchi!”+ 13 Ndipo wakamwambia: “Watumishi wako ni ndugu kumi na wawili.+ Sisi ni wana wa mtu mmoja+ tu katika nchi ya Kanaani; na tazama, yule mdogo zaidi yuko na baba yetu leo,+ naye yule mwingine hayuko.”+

14 Hata hivyo, Yosefu akawaambia: “Ni kama nilivyowaambia, nikisema: ‘Ninyi ni wapelelezi!’ 15 Hivyo ndivyo mtakavyojaribiwa. Kama Farao anavyoishi, hamtatoka hapa mpaka ndugu yenu mdogo atakapokuja hapa.+ 16 Mtumeni mmoja wenu akamlete ndugu yenu, huku ninyi mkiwa mmefungwa, ili maneno yenu yajaribiwe kama ni ya kweli.+ Ikiwa sivyo, basi, kama Farao anavyoishi, ninyi ni wapelelezi.” 17 Kisha akawatia pamoja kifungoni kwa siku tatu.

18 Baada ya hayo Yosefu akawaambia siku ya tatu. “Fanyeni hili ili mwendelee kuishi. Mimi ninamwogopa+ Mungu wa kweli. 19 Ikiwa ninyi ni wanyoofu, acheni mmoja wa ndugu zenu afungwe katika nyumba yenu ya kifungo,+ lakini ninyi wengine mwende, chukueni nafaka kwa sababu ya njaa iliyo katika nyumba zenu.+ 20 Kisha mtaniletea ndugu yenu mdogo, ili maneno yenu yaonekane kuwa yenye kutegemeka; nanyi hamtakufa.”+ Basi wakafanya hivyo.

21 Nao wakaanza kusemezana: “Bila shaka tuna hatia kuhusiana na ndugu yetu,+ kwa sababu tuliona nafsi yake ikitaabika alipotuomba kwa bidii tumwonee huruma, lakini sisi hatukusikiliza. Ndiyo sababu taabu hii imetupata.”+ 22 Kisha Rubeni akawajibu, akawaambia: “Je, sikuwaambia, ‘Msimtendee mtoto huyo dhambi,’ lakini hamkusikia?+ Na sasa damu yake inadaiwa tena.”+ 23 Lakini wao hawakujua kwamba Yosefu alikuwa akisikiliza, kwa sababu kulikuwako mtafsiri kati yao. 24 Basi akajitenga nao, akaanza kulia.+ Kisha akarudi kwao, akaongea nao, akamchukua Simeoni+ kati yao na kumfunga mbele ya macho yao.+ 25 Baada ya hayo Yosefu akatoa amri, nao wakavijaza kabisa vyombo vyao nafaka. Pia, walipaswa kurudisha pesa za watu hao kwenye gunia la kila mmoja wao+ na kuwapa vyakula kwa ajili ya safari.+ Ndivyo walivyofanyiwa.

26 Basi wakapakia nafaka yao juu ya punda zao na kuondoka huko. 27 Mmoja wao alipofungua gunia lake ili ampe punda wake chakula wakiwa mahali pa kukaa usiku,+ akaona pesa zake, na tazama, zilikuwa katika kinywa cha mfuko wake.+ 28 Basi akawaambia ndugu zake: “Pesa zangu zimerudishwa na tazama, ziko hapa mfukoni mwangu!” Ndipo mioyo yao ikazimia, hivi kwamba wakageukiana wakitetemeka,+ wakisema: “Ni nini hili Mungu ametutendea?”+

29 Mwishowe wakafika kwa Yakobo baba yao katika nchi ya Kanaani, wakamwambia mambo yote yaliyokuwa yamewapata, wakisema: 30 “Bwana wa nchi hiyo alisema nasi kwa ukali,+ kwa kuwa alituwazia kuwa sisi ni watu wanaoipeleleza nchi.+ 31 Lakini tukamwambia, ‘Sisi ni watu wanyoofu.+ Sisi si wapelelezi. 32 Sisi ni ndugu kumi na wawili,+ wana wa baba yetu.+ Mmoja hayuko,+ na yule mdogo leo yuko na baba yetu katika nchi ya Kanaani.’+ 33 Lakini huyo mtu aliye bwana wa nchi hiyo akatuambia,+ ‘Kwa njia hii nitajua kama ninyi ni wanyoofu:+ Mmoja wa ndugu zenu akae nami.+ Kisha chukueni vitu fulani kwa sababu ya njaa iliyo katika nyumba zenu, mwende.+ 34 Nanyi mkamlete ndugu yenu mdogo, ili nijue kwamba ninyi si wapelelezi bali ni watu wanyoofu. Nitawarudishia ndugu yenu, nanyi mnaweza kufanya biashara yenu nchini.’”+

35 Ikawa kwamba walipokuwa wakitoa vilivyokuwa ndani ya magunia yao tazama, kifurushi cha pesa cha kila mmoja wao kilikuwa katika gunia lake. Na wao na baba yao pia wakapata kuona vifurushi vyao vya pesa, nao wakaogopa. 36 Kisha Yakobo baba yao akawaambia: “Mmefanya mimi nifiwe!+ Yosefu hayuko naye Simeoni hayuko,+ na Benyamini mtamchukua! Mambo yote hayo yamenijia mimi!” 37 Lakini Rubeni akamwambia baba yake: “Nisipomrudisha kwako uwaue wanangu wawili.+ Nipe yeye, nami ndimi nitakayemrudisha kwako.”+ 38 Lakini, akasema: “Mwanangu hatashuka kwenda nanyi, kwa sababu ndugu yake amekufa naye amebaki peke yake.+ Tukio lenye kufisha likimpata katika njia mtakayoiendea, basi bila shaka mtazishusha mvi zangu kwa huzuni mpaka katika Kaburi.”*+

43 Nayo njaa ilikuwa kali katika nchi.+ 2 Ikawa mara tu walipokuwa wamemaliza kuila nafaka waliyokuwa wameleta kutoka Misri,+ baba yao akawaambia: “Rudini, mkatununulie chakula kidogo.”+ 3 Kisha Yuda akamwambia:+ “Yule mtu alituhakikishia waziwazi, akisema, ‘Msiuone uso wangu tena isipokuwa ndugu yenu awe pamoja nanyi.’+ 4 Ikiwa utamruhusu ndugu yetu aende nasi,+ tuko tayari kwenda kukununulia chakula. 5 Lakini ikiwa hutamruhusu aende nasi, hatutaenda, kwa sababu yule mtu alituambia, ‘Msiuone uso wangu tena isipokuwa ndugu yenu awe pamoja nanyi.’”+ 6 Naye Israeli akasema:+ “Kwa nini mmenidhuru kwa kumwambia mtu huyo ya kwamba mna ndugu mwingine?” 7 Kisha wakasema: “Mtu huyo aliuliza moja kwa moja kutuhusu na kuhusu jamaa zetu, akisema, ‘Je, baba yenu angali hai?+ Je, mna ndugu mwingine?’ nasi tukamwambia kupatana na mambo hayo.+ Tungewezaje kujua kwamba kwa hakika atasema, ‘Shukeni na ndugu yenu’?”+

8 Mwishowe Yuda akamwambia Israeli baba yake: “Mruhusu huyu mvulana aende nami,+ ili tupate kuondoka twende na ili tuendelee kuishi ili tusife,+ sisi na wewe na watoto wetu wadogo.+ 9 Mimi nitakuwa dhamana kwa ajili yake.+ Umdai mkononi mwangu.+ Nisipomrudisha kwako na kumweka mbele yako, basi nitakuwa nimekutendea dhambi ya kudumu. 10 Lakini ikiwa hatungalikawia, kufikia sasa tungalikuwa tumefika huko na kurudi mara mbili hizi.”+

11 Kisha Israeli baba yao akawaambia: “Ikiwa, basi, ndivyo ilivyo,+ fanyeni hivi: Chukueni mali bora zaidi ya nchi katika vyombo vyenu mkampelekee mtu huyo iwe zawadi:+ zeri kidogo,+ na asali kidogo,+ ubani mweusi na gome lenye utomvu,+ kungu na lozi.+ 12 Pia chukueni pesa mara mbili mkononi mwenu; na pesa zilizorudishwa katika vinywa vya mifuko yenu mzirudishe zikiwa mkononi mwenu.+ Huenda lilikuwa kosa.+ 13 Nanyi mchukueni ndugu yenu, mwondoke, mrudi kwa mtu huyo. 14 Na Mungu Mweza-Yote na awape huruma mbele ya mtu huyo,+ ili amwachilie yule ndugu yenu mwingine na Benyamini. Lakini ikiwa nitafiwa, kwa kweli nitafiwa!”+

15 Basi hao watu wakachukua zawadi hiyo, nao wakachukua pesa mara mbili mkononi mwao na Benyamini. Kisha wakaondoka na kwenda zao Misri, wakasimama mbele ya Yosefu.+ 16 Yosefu alipomwona Benyamini akiwa pamoja nao, akamwambia mara moja mtu aliyekuwa juu ya nyumba yake: “Wapeleke watu hawa nyumbani, uchinje wanyama na kufanya matayarisho,+ kwa sababu watu hawa watakula pamoja nami mchana.” 17 Bila kukawia yule mtu akafanya kama vile Yosefu alivyokuwa amesema.+ Basi akawapeleka hao watu nyumbani kwa Yosefu. 18 Lakini hao watu wakaogopa kwa sababu walikuwa wamepelekwa nyumbani kwa Yosefu,+ wakaanza kusema: “Tunaletwa hapa ili watuangukie na kutushambulia na kutuchukua tuwe watumwa na pia punda zetu kwa sababu ya pesa tulizorudi nazo katika mifuko yetu pale mwanzoni!”+

19 Kwa hiyo wakamkaribia yule mtu aliyekuwa juu ya nyumba ya Yosefu, wakaongea naye kwenye mwingilio wa nyumba hiyo, 20 nao wakasema: “Tunakuomba radhi, bwana wangu! Kwa kweli mwanzoni tulikuja kununua chakula.+ 21 Lakini ikatukia kwamba tulipofika mahali pa kulala+ na kuanza kufungua mifuko yetu, kumbe, pesa za kila mmoja wetu zilikuwa katika kinywa cha mfuko wake, pesa zetu zikiwa na uzani wake kamili. Kwa hiyo tungependa kuzirudisha kwa mikono yetu wenyewe.+ 22 Nasi tumeleta pesa zaidi mikononi mwetu ili kununua chakula. Kwa hakika hatujui ni nani aliyeziweka pesa zetu mifukoni mwetu.”+ 23 Kisha akasema: “Mambo ni sawa kwenu. Msiogope.+ Mungu wenu na Mungu wa baba yenu aliwapa hazina mifukoni mwenu.+ Pesa zenu zilinifikia kwanza.” Kisha akamleta Simeoni kwao.+

24 Basi yule mtu akawaleta nyumbani kwa Yosefu, akawapa maji wapate kuoshwa miguu yao,+ naye akawapa chakula kwa ajili ya punda zao.+ 25 Nao wakaitayarisha zawadi+ kwa ajili ya Yosefu atakapokuja mchana, kwa sababu walikuwa wamesikia kwamba hapo ndipo wangekula mkate.+ 26 Yosefu alipoingia nyumbani, wakampelekea zawadi iliyokuwa mkononi mwao ndani ya nyumba, wakajilaza chini kifudifudi mbele yake.+ 27 Kisha akawauliza hali yao na kusema:+ “Je, baba yenu, yule mzee mliyesema juu yake, anaendelea vema? Je, angali hai?”+ 28 Wakajibu, wakasema: “Mtumishi wako baba yetu anaendelea vema. Angali hai.” Kisha wakainama na kulala kifudifudi.+

29 Alipoinua macho yake na kumwona Benyamini ndugu yake, mwana wa mama yake,+ akasema: “Je, huyu ni ndugu yenu, yule mdogo zaidi mliyeniambia juu yake?”+ Naye akaongeza kusema: “Mungu na akuonyeshe kibali chake,+ mwanangu.” 30 Sasa Yosefu alikuwa akiharakisha, kwa sababu hisia zake za ndani zilianza kusisimuka kumwelekea ndugu yake,+ hata akatafuta mahali pa kulilia, naye akaingia katika chumba cha ndani, akaanza kulia machozi humo.+ 31 Kisha akanawa uso wake, akatoka, akajizuia, akasema:+ “Leteni chakula.”+ 32 Nao wakamletea chakula chake kando na kile chao kando na cha Wamisri waliokuwa wakila naye kando; kwa maana Wamisri hawangeweza kula chakula pamoja na Waebrania, kwa sababu hilo ni chukizo kwa Wamisri.+

33 Nao walikuwa wameketi mbele yake, mzaliwa wa kwanza kupatana na haki ya mzaliwa wa kwanza+ naye yule mdogo zaidi kupatana na uchanga wake; na hao watu wakawa wakitazamana kwa mshangao. 34 Naye akawa akituma watu wachukue visehemu vya chakula kutoka mbele yake na kuwapelekea, lakini akawa akiongeza kisehemu cha Benyamini mara tano kuliko visehemu vya wale wengine wote.+ Basi wakaendelea kula karamu na kunywa naye mpaka waliposhiba.+

44 Baadaye akamwamuru mtu aliyekuwa akisimamia nyumba yake,+ akisema: “Ijaze mifuko ya watu hawa kwa chakula kwa kadiri wanavyoweza kuchukua. Utie pesa za kila mmoja wao katika kinywa cha mfuko wake.+ 2 Lakini kiweke kikombe changu, kile kikombe cha fedha, katika kinywa cha mfuko wa yule mdogo zaidi pamoja na pesa za nafaka yake.” Basi akafanya kupatana na neno la Yosefu alilokuwa amesema.+

3 Asubuhi kulikuwa kumepambazuka watu hao waliporuhusiwa kuondoka,+ pamoja na punda zao. 4 Wakatoka nje ya jiji. Hawakuwa wameenda mbali wakati Yosefu alipomwambia mtu aliyekuwa akisimamia nyumba yake: “Ondoka! Wafuatilie watu hao nawe uhakikishe umewafikia na kuwaambia, ‘Kwa nini mmelipa ubaya kwa wema?+ 5 Je, kikombe hiki sicho anachonywea bwana wangu na ambacho hutumia kusoma ishara za bahati kwa ustadi?+ Mmefanya kitendo kibaya.’”

6 Mwishowe akawafikia na kuwaambia maneno hayo. 7 Lakini wakamwambia: “Kwa nini bwana wangu anasema maneno kama hayo? Ni jambo lisilowaziwa kwamba watumishi wako wafanye lolote kama hilo. 8 Kwani, pesa tulizopata vinywani mwa mifuko yetu tulikurudishia kutoka nchi ya Kanaani.+ Basi, tungewezaje kuiba fedha au dhahabu katika nyumba ya bwana wako?+ 9 Mtumwa wako atakayepatikana nacho na afe, nasi tuwe watumwa kwa bwana wangu.”+ 10 Ndipo akasema: “Basi sasa na iwe hivyo kama mlivyosema.+ Yule ambaye atapatikana kuwa nacho atakuwa mtumwa wangu,+ lakini ninyi mtakuwa hamna hatia.” 11 Kisha wakashusha chini upesi kila mmoja mfuko wake nao wakafungua kila mtu mfuko wake. 12 Naye akatafuta kwa uangalifu. Akaanzia kwa yule mkubwa zaidi na kumalizia kwa yule mdogo zaidi. Mwishowe kikombe kikapatikana katika mfuko wa Benyamini.+

13 Kisha wakararua nguo zao za kujitanda,+ na kila mmoja akainua mzigo wake na kuurudisha juu ya punda wake, wakarudi jijini. 14 Naye Yuda+ na ndugu zake wakaenda mpaka nyumbani kwa Yosefu, naye bado alikuwamo; nao wakaanguka chini mbele yake.+ 15 Yosefu akawaambia: “Ni tendo gani hili mlilolifanya? Je, hamkujua kwamba mimi naweza kusoma ishara za bahati kwa ustadi?”+ 16 Yuda akajibu, akasema: “Tumwambie nini bwana wangu? Tuseme nini? Nasi tunaweza kuonyeshaje kuwa sisi ni waadilifu?+ Mungu wa kweli amegundua kosa la watumwa wako.+ Tazama sisi ni watumwa wa bwana wangu,+ sisi na yule ambaye mkononi mwake kikombe kilipatikana!” 17 Lakini yeye akasema: “Ni jambo lisilowaziwa upande wangu kufanya hivyo!+ Mtu ambaye mkononi mwake kikombe hicho kilipatikana ndiye atakayekuwa mtumwa wangu.+ Ninyi wengine, nendeni kwa amani kwa baba yenu.”+

18 Sasa Yuda akamkaribia, akamwambia: “Nakuomba, bwana wangu, tafadhali mruhusu mtumwa wako aongee neno masikioni mwa bwana wangu,+ wala usiache hasira+ yako iwake juu ya mtumwa wako, kwa sababu wewe ni kama Farao.+ 19 Bwana wangu aliwauliza watumwa wake, akisema, ‘Je, mna baba au ndugu?’ 20 Basi tukamwambia bwana wangu, ‘Tuna baba aliye mzee na mtoto wa uzee wake, aliye mdogo zaidi.+ Lakini ndugu yake amekufa hivi kwamba yeye tu ndiye aliyesalia wa mama yake,+ na baba yake anampenda.’ 21 Kisha ukawaambia watumwa wako, ‘Mleteni kwangu nipate kumwona.’+ 22 Lakini tukamwambia bwana wangu, ‘Mvulana huyo hawezi kumwacha baba yake. Akimwacha, bila shaka baba yake atakufa.’+ 23 Halafu ukawaambia watumwa wako, ‘Ndugu yenu mdogo asiposhuka pamoja nanyi, msiuone uso wangu tena kamwe.’+

24 “Basi tukaenda kwa mtumwa wako, baba yangu, tukamwambia maneno ya bwana wangu. 25 Baadaye baba yetu akasema, ‘Rudini, mkatununulie chakula kidogo.’+ 26 Lakini tukamwambia, ‘Hatuwezi kwenda. Ikiwa ndugu yetu mdogo yuko pamoja nasi tutaenda, kwa sababu hatuwezi kuuona uso wa mtu huyo ikiwa ndugu yetu mdogo hayuko pamoja nasi.’+ 27 Kisha mtumwa wako, baba yangu, akatuambia, ‘Ninyi wenyewe mnajua vizuri kwamba mke wangu alinizalia wana wawili tu.+ 28 Baadaye mmoja aliniacha nami nikasema: “Ah, haikosi ameraruliwa vipande-vipande!”+ nami sijamwona mpaka leo hii. 29 Mkimchukua huyu naye toka machoni pangu na apatwe na tukio lenye kufisha, bila shaka mtazishusha mvi zangu kwa msiba mpaka katika Kaburi.’*+

30 “Sasa basi, nikifika tu kwa mtumwa wako, baba yangu, bila mvulana huyu, na hali nafsi yake imeshikamana na nafsi ya mvulana huyu,+ 31 basi bila shaka itatukia kwamba mara atakapoona kwamba huyu mvulana hayupo atakufa tu, na watumwa wako kwa kweli watazishusha mvi za mtumwa wako baba yetu kwa huzuni mpaka katika Kaburi.* 32 Kwa maana mtumwa wako alijitoa kuwa dhamana+ ya mvulana huyu awapo mbali na baba yake, akisema, ‘Nisipomrudisha kwako, basi nitakuwa nimemtendea baba yangu dhambi milele.’+ 33 Tafadhali sasa, basi, mtumwa wako na abaki akiwa mtumwa badala ya huyu mvulana ili apate kwenda na ndugu zake.+ 34 Kwa maana ninawezaje kwenda kwa baba yangu bila yeye nisije nikautazama msiba utakaompata baba yangu?”+

45 Hapo Yosefu hakuweza kujizuia tena mbele ya wote waliokuwa wamesimama karibu naye.+ Basi akapaaza sauti: “Mwondoeni kila mtu kutoka kwangu!” Wala hakuna mtu mwingine yeyote aliyesimama pamoja naye alipojitambulisha kwa ndugu zake.+

2 Naye akaanza kupaaza sauti yake akilia,+ hivi kwamba Wamisri wakaisikia na nyumba ya Farao ikaisikia. 3 Mwishowe Yosefu akawaambia ndugu zake: “Mimi ni Yosefu. Je, baba yangu angali hai?” Lakini ndugu zake hawakuweza kumjibu kamwe, kwa sababu waliingiwa na wasiwasi kwa sababu yake.+ 4 Basi Yosefu akawaambia ndugu zake: “Tafadhali, nikaribieni.” Basi wakamkaribia.

Kisha akawaambia: “Mimi ni Yosefu ndugu yenu, mliyemuuza Misri.+ 5 Lakini sasa msihuzunike+ wala msijikasirikie kwa sababu mliniuza huku; kwa sababu Mungu alinituma mbele yenu ili kuhifadhi uhai.+ 6 Kwa maana huu ni mwaka wa pili wa njaa duniani,+ na bado kuna miaka mitano ambayo hakutakuwa na wakati wa kulima wala mavuno.+ 7 Kwa sababu hiyo Mungu alinituma mbele yenu ili niwawekee ninyi mabaki+ duniani na kuwaweka hai kwa wokovu mkubwa. 8 Basi sasa si ninyi ambao mlinileta hapa,+ ila ni Mungu wa kweli, ili aniweke niwe baba+ kwa Farao na bwana kwa nyumba yake yote na kuwa mtawala katika nchi yote ya Misri.

9 “Nendeni upesi kwa baba yangu, mkamwambie, ‘Hivi ndivyo mwana wako Yosefu amesema: “Mungu ameniweka kuwa bwana wa nchi yote ya Misri.+ Njoo kwangu. Usikawie. 10 Ukae katika nchi ya Gosheni,+ uishi karibu nami, wewe na wana wako na wana wa wana wako na makundi yako na mifugo yako na kila kitu ulicho nacho. 11 Nami nitakupa chakula huko, kwa maana bado kuna miaka mitano ya njaa;+ usije kuwa maskini wewe na nyumba yako na kila kitu ulicho nacho.’” 12 Na tazama, macho yenu na macho ya ndugu yangu Benyamini yanaona ya kwamba ni kinywa changu kinachosema nanyi.+ 13 Basi msikose kumwambia baba yangu juu ya utukufu wangu wote katika Misri na kila kitu ambacho mmeona; nanyi mfanye haraka kumleta baba yangu hapa.”

14 Kisha akamwangukia Benyamini shingoni na kuanza kulia, naye Benyamini akalia shingoni pake.+ 15 Akawabusu ndugu zake wote akawalilia,+ kisha ndugu zake wakaongea naye.

16 Habari hizo zikasikiwa nyumbani kwa Farao, ikisemekana: “Ndugu za Yosefu wamekuja!” Ikawa vema machoni pa Farao na watumishi wake.+ 17 Basi Farao akamwambia Yosefu: “Waambie ndugu zako, ‘Fanyeni hivi: Wapakieni wanyama wenu wa kubeba mizigo mwingie nchi ya Kanaani,+ 18 mchukue baba yenu na watu wa nyumba zenu mje hapa kwangu, niwape mema ya nchi ya Misri; na mle unono wa nchi.+ 19 Na wewe mwenyewe unaamriwa:+ “Fanyeni hivi: Jichukulieni magari ya kukokotwa+ kutoka nchi ya Misri kwa ajili ya watoto wenu na wake zenu, mkamchukue baba yenu katika gari moja mje hapa.+ 20 Na jicho lenu lisihuzunikie vifaa vyenu,+ kwa sababu wema wa nchi yote ya Misri ni wenu.”’”+

21 Kisha wana wa Israeli wakafanya hivyo, naye Yosefu akawapa magari kama Farao alivyoamuru, pia akawapa vyakula+ vya njiani. 22 Akampa kila mmoja wao nguo moja ya kujitanda ya kubadili,+ lakini akampa Benyamini vipande mia tatu vya fedha na nguo tano za kujitanda za kubadili.+ 23 Na akampelekea baba yake vitu hivi: punda kumi waliochukua vitu vyema vya Misri na punda-jike kumi waliochukua nafaka na mkate na riziki kwa ajili ya baba yake njiani. 24 Basi akawaaga ndugu zake, nao wakaenda. Hata hivyo, akawaambia: “Msigombane njiani.”+

25 Nao wakaanza kutoka Misri na mwishowe wakaingia nchi ya Kanaani kwa Yakobo baba yao. 26 Kisha wakampasha habari, wakimwambia: “Yosefu angali hai, naye ndiye anayetawala nchi yote ya Misri!”+ Lakini moyo wake ukafa ganzi, kwa sababu hakuwaamini.+ 27 Walipoendelea kumwambia maneno yote ya Yosefu aliyokuwa amewaambia na alipoona magari ambayo Yosefu alikuwa ametuma yamchukue, roho ya Yakobo baba yao ikaanza kufufuka.+ 28 Kisha Israeli akasema: “Inatosha! Yosefu mwanangu angali hai! Ah, acha niende nikamwone kabla sijafa!”+

46 Basi Israeli na wote waliokuwa wake wakaondoka, wakafika Beer-sheba+ naye akamtolea dhabihu Mungu wa baba yake Isaka.+ 2 Kisha Mungu akaongea na Israeli katika maono ya usiku, na kumwambia:+ “Yakobo, Yakobo!” naye akajibu, akasema: “Mimi hapa!”+ 3 Naye akaendelea kusema: “Mimi ndiye Mungu wa kweli,+ Mungu wa baba yako.+ Usiogope kwenda Misri, kwa maana nitakufanya uwe taifa kubwa huko.+ 4 Mimi mwenyewe nitashuka pamoja nawe Misri nami nitakupandisha pia;+ na Yosefu ataweka mkono wake juu ya macho yako.”+

5 Kisha Yakobo akaondoka Beer-sheba, nao wana wa Israeli wakaendelea kumsafirisha Yakobo baba yao na watoto wao na wake zao katika magari ambayo Farao alikuwa ametuma yamsafirishe.+ 6 Tena, wakachukua mifugo yao na mali zao, walizokuwa wamekusanya katika nchi ya Kanaani.+ Mwishowe wakafika Misri, Yakobo na uzao wake wote pamoja naye. 7 Aliwaleta wanawe na wana wa wanawe pamoja naye, binti zake na binti za wanawe, naam, uzao wake wote, pamoja naye, wakaingia Misri.+

8 Sasa haya ndiyo majina ya wana wa Israeli waliokuja Misri:+ Yakobo na wanawe: mzaliwa wa kwanza wa Yakobo alikuwa Rubeni.+

9 Na wana wa Rubeni walikuwa Hanoki na Palu na Hezroni na Karmi.+

10 Na wana wa Simeoni+ walikuwa Yemueli na Yamini na Ohadi na Yakini+ na Zohari na Shauli+ mwana wa mwanamke Mkanaani.

11 Na wana wa Lawi+ walikuwa Gershoni,+ Kohathi+ na Merari.+

12 Na wana wa Yuda+ walikuwa Eri+ na Onani+ na Shela+ na Perezi+ na Zera.+ Lakini Eri na Onani walikufa katika nchi ya Kanaani.+

Na wana wa Perezi wakawa ni Hezroni+ na Hamuli.+

13 Na wana wa Isakari+ walikuwa Tola+ na Puva+ na Iobu na Shimroni.+

14 Na wana wa Zabuloni+ walikuwa Seredi na Eloni na Yahleeli.+

15 Hawa ndio wana wa Lea,+ aliomzalia Yakobo huko Padan-aramu, na binti yake Dina.+ Nafsi zote za wanawe na za binti zake zilikuwa ni 33.

16 Na wana wa Gadi+ walikuwa Zifioni na Hagi na Shuni na Esboni, Eri na Arodi na Areli.+

17 Na wana wa Asheri+ walikuwa Imna na Ishva na Ishvi na Beria,+ na Sera dada yao.

Na wana wa Beria walikuwa Heberi na Malkieli.+

18 Hao ndio wana wa Zilpa,+ ambaye Labani alimpa binti yake Lea. Mwishowe akamzalia Yakobo hao: nafsi 16.

19 Wana wa Raheli,+ mke wa Yakobo, walikuwa Yosefu+ na Benyamini.+

20 Na katika nchi ya Misri Yosefu alizaa, Manase+ na Efraimu,+ ambao Asenathi+ binti ya Potifera kuhani wa Oni alimzalia.

21 Na wana wa Benyamini walikuwa Bela+ na Bekeri+ na Ashbeli, Gera+ na Naamani,+ Ehi na Roshi, Mupimu+ na Hupimu+ na Ardi.

22 Hao ndio wana wa Raheli ambao alimzalia Yakobo. Nafsi zote zilikuwa 14.

23 Na wana wa Dani+ walikuwa Hushimu.+

24 Na wana wa Naftali+ walikuwa Yahzeeli na Guni+ na Yezeri na Shilemu.+

25 Hao ndio wana wa Bilha,+ ambaye Labani alimpa Raheli binti yake. Mwishowe akamzalia Yakobo hao; nafsi zote zilikuwa 7.

26 Nafsi zote zilizomjia Yakobo na kuingia Misri zilikuwa zile zilizotoka kiunoni mwake,+ mbali na wake za wana wa Yakobo. Nafsi zote zilikuwa 66. 27 Na wana wa Yosefu aliowazaa akiwa Misri walikuwa nafsi 2. Nafsi zote za nyumba ya Yakobo zilizokuja Misri zilikuwa 70.+

28 Naye akamtuma Yuda+ mbele yake kwa Yosefu ili atoe habari kabla yake Gosheni. Kisha wakaingia nchi ya Gosheni.+ 29 Ndipo Yosefu akatayarisha gari lake, akaenda kumpokea baba yake Israeli huko Gosheni.+ Alipomtokea, akamwangukia shingoni mara moja, akalia shingoni pake tena na tena.+ 30 Mwishowe Israeli akamwambia Yosefu: “Sasa niko tayari kufa,+ kwa kuwa nimeuona uso wako, kwa maana ungali hai.”

31 Kisha Yosefu akawaambia ndugu zake na watu wa nyumba ya baba yake: “Acheni niende nikamwarifu Farao, nimwambie,+ ‘Ndugu zangu na watu wa nyumba ya baba yangu waliokuwa katika nchi ya Kanaani wamekuja hapa kwangu.+ 32 Na hao watu ni wachungaji,+ kwa sababu walikuwa wafugaji;+ nayo makundi yao na mifugo yao yote waliyo nayo wameleta huku.’+ 33 Na itatukia kwamba Farao anapowaita na kuwauliza, ‘Mnafanya kazi gani?’ 34 Mtasema, ‘Watumishi wako wamekuwa wafugaji sikuzote tangu ujana wetu mpaka sasa, sisi na pia mababu zetu,’+ ili mpate kuishi katika nchi ya Gosheni,+ kwa sababu kila mchungaji wa kondoo ni chukizo katika nchi ya Misri.”+

47 Basi Yosefu akaenda, akampa Farao habari, na kusema:+ “Baba yangu na ndugu zangu na makundi yao na mifugo yao na vyote walivyo navyo, wamekuja kutoka nchi ya Kanaani, na tazama, wako katika nchi ya Gosheni.”+ 2 Naye akatwaa watu watano kutoka kati ya ndugu zake wote apate kuwapeleka mbele ya Farao.+

3 Kisha Farao akawauliza ndugu zake: “Mnafanya kazi gani?”+ Basi wakamwambia Farao: “Watumishi wako ni wachungaji wa kondoo,+ sisi na mababu zetu pia.”+ 4 Kisha wakamwambia Farao: “Tumekuja kukaa tukiwa wageni nchini,+ kwa sababu hakuna malisho kwa ajili ya makundi waliyo nayo watumishi wako,+ kwa maana njaa ni kali katika nchi ya Kanaani.+ Na sasa, tafadhali, waruhusu watumishi wako wakae katika nchi ya Gosheni.”+ 5 Ndipo Farao akamwambia Yosefu: “Baba yako na ndugu zako wamekujia hapa. 6 Nchi ya Misri iko chini ya mamlaka yako.+ Wape makao baba yako na ndugu zako katika sehemu bora kabisa ya nchi.+ Wape makao katika nchi ya Gosheni,+ na ikiwa unajua kwamba kati yao mna watu walio hodari,+ uwaweke kuwa wakuu wa mifugo yangu.”+

7 Kisha Yosefu akamwingiza Yakobo baba yake, akamjulisha kwa Farao, naye Yakobo akambariki Farao.+ 8 Sasa Farao akamuuliza Yakobo: “Siku za miaka ya maisha yako ni ngapi?” 9 Basi Yakobo akamwambia Farao: “Siku za miaka ya makao yangu katika nchi ya kigeni ni miaka 130.+ Zimekuwa chache na zenye kutaabisha,+ nazo hazijafikia siku za miaka ya maisha ya baba zangu, siku za makao yao katika nchi ya kigeni.”+ 10 Halafu Yakobo akambariki Farao na kuondoka mbele ya Farao.+

11 Kwa hiyo Yosefu akampa baba yake na ndugu zake makao, naye akawapa mali katika nchi ya Misri, katika sehemu bora kabisa ya nchi hiyo, katika nchi ya Ramesesi,+ kama vile tu Farao alivyokuwa ameamuru. 12 Na Yosefu akaendelea kumpa mkate baba yake na ndugu zake na watu wote wa nyumba ya baba yake,+ kwa kadiri ya idadi ya watoto.+

13 Sasa hapakuwa na mkate katika nchi yote, kwa sababu njaa ilikuwa kali sana;+ nayo nchi ya Misri na nchi ya Kanaani zikaishiwa kabisa kwa sababu ya hiyo njaa.+ 14 Yosefu akakusanya pesa zote zilizopatikana katika nchi ya Misri na katika nchi ya Kanaani za nafaka ambayo watu walikuwa wakinunua;+ naye akawa akizileta pesa hizo nyumbani kwa Farao. 15 Mwishowe pesa za nchi ya Misri na za nchi ya Kanaani zikaisha, na Wamisri wote wakaanza kumjia Yosefu, wakisema: “Tupe mkate!+ Na kwa nini tufe mbele yako kwa kuwa pesa zimekwisha?”+ 16 Kisha Yosefu akasema: “Leteni mifugo yenu nami nitawapa mkate kwa kubadilishana na mifugo yenu, ikiwa pesa zimekwisha.” 17 Nao wakaanza kumletea Yosefu mifugo yao; naye Yosefu akawapa mkate kwa kubadilishana na farasi zao na makundi na mifugo na punda,+ naye akawapa mkate kwa kubadilishana na mifugo yao yote mwaka huo.

18 Mwishowe mwaka huo ukamalizika, nao wakaanza kumjia mwaka uliofuata na kumwambia: “Hatutamficha bwana wangu lakini pesa na makundi ya wanyama wa kufugwa wameishia kwa bwana wangu.+ Hakuna kinachosalia mbele ya bwana wangu ila miili yetu na mashamba yetu.+ 19 Kwa nini tufe machoni pako,+ sisi na mashamba yetu pia? Utununue sisi na mashamba yetu kwa mkate,+ nasi pamoja na mashamba yetu tutakuwa watumwa wa Farao; na utupe mbegu ili tupate kuishi na ili tusife na mashamba yetu yasikae ukiwa.”+ 20 Basi Yosefu akamnunulia Farao mashamba yote ya Wamisri,+ kwa sababu Wamisri waliuza kila mtu shamba lake, kwa maana ile njaa ilikuwa imewalemea sana; na hayo mashamba yakawa ya Farao.

21 Naye akawaondoa watu na kuwapeleka majijini toka mwisho mmoja wa eneo la Misri mpaka mwisho ule mwingine.+ 22 Ni mashamba ya makuhani tu ndiyo hakuyanunua,+ kwa sababu posho ya makuhani ilitoka kwa Farao, nao walikula posho yao waliyopewa na Farao.+ Ndiyo sababu hawakuyauza mashamba yao.+ 23 Kisha Yosefu akawaambia watu: “Tazameni, leo nimewanunua ninyi na mashamba yenu kwa ajili ya Farao. Mbegu zenu hizi, zipandeni katika mashamba.+ 24 Wakati ambapo zitazaa,+ ndipo mtampa Farao sehemu ya tano,+ lakini sehemu nne zitakuwa zenu, ziwe mbegu za shamba na chakula chenu na cha wale walio katika nyumba zenu na cha watoto wenu.”+ 25 Basi wakasema: “Umehifadhi uhai wetu.+ Na tupate kibali machoni pako bwana wangu, nasi tutakuwa watumwa wa Farao.”+ 26 Na Yosefu akaifanya iwe amri mpaka leo hii kuhusu mashamba yaliyo mali ya Misri ya kwamba Farao apewe mpaka sehemu ya tano. Ni mashamba ya makuhani tu wakiwa kikundi tofauti ndiyo hayakuwa ya Farao.+

27 Na Israeli akaendelea kukaa katika nchi ya Misri, katika nchi ya Gosheni;+ nao wakafanya makao humo, wakaongezeka, wakawa wengi sana.+ 28 Na Yakobo akaendelea kuishi katika nchi ya Misri kwa miaka 17, hivi kwamba siku za miaka ya maisha ya Yakobo zikawa miaka 147.+

29 Mwishowe siku za Israeli kufa zikakaribia.+ Basi akamwita mwana wake Yosefu, akamwambia: “Ikiwa sasa nimepata kibali machoni pako, tafadhali, weka mkono wako chini ya paja langu,+ nawe unionyeshe fadhili zenye upendo na kweli.+ (Tafadhali, usinizike Misri.)+ 30 Nami nitalala pamoja na baba zangu,+ nawe unichukue toka Misri, unizike katika kaburi lao.”+ Basi akasema: “Mimi mwenyewe nitafanya kama ulivyosema.” 31 Kisha akamwambia: “Niapie.” Basi akamwapia.+ Ndipo Israeli akajilaza kifudifudi juu ya kichwa cha kitanda.+

48 Ikawa kwamba baada ya mambo hayo Yosefu akaambiwa: “Tazama, baba yako anadhoofika.” Basi akawachukua wanawe wawili Manase na Efraimu,+ pamoja naye. 2 Kisha Yakobo akaambiwa: “Tazama, mwana wako Yosefu amekuja kwako.” Basi Israeli akajikaza akaketi kitandani mwake. 3 Naye Yakobo akamwambia Yosefu:

“Mungu Mweza-Yote alinitokea Luzi+ katika nchi ya Kanaani apate kunibariki.+ 4 Naye akaniambia, ‘Tazama, nakufanya uzae,+ nami nitakufanya kuwa wengi na nitakufanya uwe kutaniko la vikundi vya watu,+ nami nitaupa uzao wako baada yako nchi hii iwe miliki mpaka wakati usio na kipimo.’+ 5 Na sasa wana wako wawili waliozaliwa katika nchi ya Misri kabla sijaja hapa kwako Misri ni wangu.+ Efraimu na Manase watakuwa wangu kama vile Rubeni na Simeoni.+ 6 Lakini watoto wako utakaozaa baada ya hawa watakuwa wako. Pamoja na majina ya ndugu zao wataitwa katika urithi wao.+ 7 Nami, nilipokuwa nikija kutoka Padani,+ Raheli alikufa+ kando yangu njiani katika nchi ya Kanaani wakati kulipokuwa kungali mwendo mkubwa kabla ya kufika Efrathi,+ basi nikamzika huko kwenye njia ya kwenda Efrathi, yaani, Bethlehemu.”+

8 Kisha Israeli akawaona wana wa Yosefu, akauliza: “Ni nani hawa?”+ 9 Yosefu akamwambia baba yake: “Hawa ndio wanangu ambao Mungu amenipa nikiwa mahali hapa.”+ Basi akasema: “Tafadhali, walete kwangu nipate kuwabariki.”+ 10 Sasa macho ya Israeli yalikuwa yamefifia kutokana na uzee.+ Hakuweza kuona. Basi akawaleta karibu naye, naye akawabusu na kuwakumbatia.+ 11 Na Israeli akamwambia Yosefu: “Sikuwaza ningeuona uso wako,+ lakini tazama, Mungu ameniruhusu nione uzao wako pia.” 12 Kisha Yosefu akawatoa katika magoti yake, naye akainama kifudifudi.+

13 Yosefu akawachukua sasa wote wawili, Efraimu kwa mkono wake wa kuume ukiwa upande wa mkono wa kushoto wa Israeli,+ na Manase kwa mkono wake wa kushoto ukiwa upande wa mkono wa kuume wa Israeli,+ akawaleta karibu naye. 14 Lakini, Israeli akaunyoosha mkono wake wa kuume na kuuweka juu ya kichwa cha Efraimu,+ ingawa ndiye aliyekuwa mdogo,+ nao mkono wake wa kushoto juu ya kichwa cha Manase.+ Aliiweka mikono yake hivyo kwa makusudi, kwa kuwa Manase ndiye aliyekuwa mzaliwa wa kwanza.+ 15 Naye akambariki Yosefu na kusema:+

“Mungu wa kweli ambaye mbele zake baba zangu Abrahamu na Isaka walitembea,+

Mungu wa kweli ambaye amekuwa akinichunga maisha yangu yote mpaka leo hii,+

16 Malaika ambaye amekuwa akiniponya katika misiba yote,+ awabariki wavulana hawa.+

Na jina langu liitwe juu yao na pia jina la baba zangu, Abrahamu na Isaka,+

Na waongezeke wawe wengi katikati ya dunia.”+

17 Yosefu alipoona kwamba baba yake aliuweka mkono wake wa kuume juu ya kichwa cha Efraimu, hakupendezwa,+ naye akajaribu kuushika mkono wa baba yake auondoe juu ya kichwa cha Efraimu na kuuweka juu ya kichwa cha Manase.+ 18 Kwa hiyo Yosefu akamwambia baba yake: “Sivyo, baba yangu, kwa sababu huyu ndiye mzaliwa wa kwanza.+ Uweke mkono wako wa kuume juu ya kichwa chake.” 19 Lakini baba yake akaendelea kukataa, akisema: “Najua, mwanangu, najua. Yeye pia atakuwa kikundi cha watu naye pia atakuwa mkuu.+ Lakini, ndugu yake mdogo atakuwa mkuu kuliko yeye,+ nao uzao wake utakuwa hesabu kamili ya mataifa.”+ 20 Naye akaendelea kuwabariki siku hiyo,+ akisema:

“Kupitia kwako Israeli na atangaze baraka tena na tena, akisema,

‘Mungu na akufanye wewe uwe kama Efraimu na kama Manase.’”+

Hivyo akaendelea kumweka Efraimu mbele ya Manase.+

21 Kisha Israeli akamwambia Yosefu: “Tazama, ninakufa,+ lakini Mungu pasipo shaka ataendelea kuwa nanyi na kuwarudisha ninyi katika nchi ya mababu zenu.+ 22 Nami, ninakupa sehemu moja ya nchi zaidi kuliko ndugu zako,+ ambayo niliichukua kutoka katika mkono wa Waamori, kwa upanga wangu na kwa upinde wangu.”

49 Baadaye Yakobo akawaita pamoja wanawe, akasema: “Jikusanyeni pamoja niwaambie yatakayowapata siku za mwisho. 2 Jikusanyeni msikilize, ninyi wana wa Yakobo, ndiyo, msikilizeni Israeli baba yenu.+

3 “Rubeni, wewe ndiwe mzaliwa wangu wa kwanza,+ nguvu zangu na mwanzo wa nguvu zangu za uzazi,+ ubora wa heshima na ubora wa nguvu. 4 Umeruka mpaka kama maji, basi usiwe na ukuu,+ kwa sababu umekipanda kitanda cha baba yako.+ Wakati huo ulikinajisi kitanda changu.+ Alikipanda!

5 “Simeoni na Lawi ni ndugu.+ Silaha zao za kuchinjia ni vyombo vya jeuri.+ 6 Ee nafsi yangu, usiingie katika kikundi chao cha rafiki.+ Ee mwelekezo wangu, usiungane na kutaniko lao,+ kwa sababu katika hasira yao waliwaua watu,+ na katika udhalimu wao walikata mishipa ya ng’ombe-dume. 7 Na ilaaniwe hasira yao,+ kwa sababu ni katili,+ na ghadhabu yao, kwa sababu hutenda kwa ukali.+ Acheni niwagawanye katika Yakobo na kuwatawanya katika Israeli.+

8 “Yuda,+ nawe, ndugu zako watakusifu.+ Mkono wako utakuwa katika kikosi cha adui zako.+ Wana wa baba yako watajilaza kifudifudi mbele yako.+ 9 Yuda ni mwana-simba.+ Mwanangu, utapanda kutoka mawindoni. Aliinama, alijinyoosha kama simba, na kama simba, ni nani anayethubutu kumwamsha?+ 10 Fimbo ya enzi haitageuka kando kutoka kwa Yuda,+ wala fimbo ya kiongozi kutoka katikati ya miguu yake, mpaka Shilo aje;+ na vikundi vya watu vitamtii yeye.+ 11 Kwa kumfunga punda wake mkomavu kwenye mzabibu na mwana-punda wake mwenyewe kwenye mzabibu mzuri, yeye kwa hakika atafua mavazi yake katika divai na vazi lake katika damu ya zabibu.+ 12 Macho yake ni mekundu kwa divai, na weupe wa meno yake unatokana na maziwa.

13 “Zabuloni atakaa kando ya bahari,+ naye atakuwa kando ya bahari ambapo meli hukaa zikiwa zimetia nanga;+ na sehemu yake ya mbali itakuwa kuelekea Sidoni.+

14 “Isakari+ ni punda mwenye mifupa migumu, aliyelala katikati ya matandiko yenye mifuko miwili. 15 Naye ataona kwamba mahali pa kupumzika ni pazuri na kwamba nchi ni yenye kupendeza; naye atainamisha bega lake abebe mizigo naye atalazimishwa kufanya kazi ya kitumwa.

16 “Dani atawahukumu watu wake akiwa mmoja wa makabila ya Israeli.+ 17 Dani na awe nyoka kando ya barabara, nyoka-bafe kando ya njia, anayeuma visigino vya farasi hivi kwamba mpandaji wake anaanguka nyuma.+ 18 Kwa kweli nitaungoja wokovu kutoka kwako, Ee Yehova.+

19 “Naye Gadi, atavamiwa na kikundi cha waporaji, lakini yeye atavamia upande wa nyuma kabisa.+

20 “Kutoka Asheri mkate wake utakuwa mnono,+ naye atatoa vitu bora vya mfalme.+

21 “Naftali+ ni paa mwembamba. Anatoa maneno ya kupendeza.+

22 “Yosefu ni chipukizi la mti unaozaa matunda,+ chipukizi la mti unaozaa matunda kando ya chemchemi,+ ambao husukuma mbele matawi yake juu ya ukuta.+ 23 Lakini wapiga-mishale waliendelea kumsumbua na kumfyatulia mishale na kuendelea kudumisha uadui kumwelekea.+ 24 Na hata hivyo upinde wake ulikuwa katika mahali pa kudumu,+ na nguvu za mikono yake zilikuwa zenye kunepa.+ Kwa mikono ya Mwenye Nguvu wa Yakobo,+ hapo ndipo alipo Mchungaji, Jiwe la Israeli.+ 25 Yeye ametoka kwa Mungu wa baba yako,+ naye atakusaidia;+ naye yuko pamoja na Mweza-Yote,+ naye atakubariki kwa baraka za mbingu zilizo juu,+ kwa baraka za kilindi cha maji kilicho chini,+ kwa baraka za maziwa na tumbo la uzazi.+ 26 Baraka za baba yako kwa kweli zitakuwa kuu kuliko baraka za milima ya milele,+ kuliko pambo la vilima vinavyodumu mpaka wakati usio na kipimo.+ Zitaendelea kuwa juu ya kichwa cha Yosefu, ndiyo, juu ya utosi wa kichwa cha yule aliyetengwa na ndugu zake.+

27 “Benyamini ataendelea kurarua kama mbwa-mwitu.+ Asubuhi atakula mnyama aliyekamatwa na jioni atagawanya nyara.”+

28 Yote hayo ndiyo makabila kumi na mawili ya Israeli, na hayo ndiyo maneno ambayo baba yao aliwaambia alipokuwa akiwabariki. Alimbariki kila mmoja kupatana na baraka yake.+

29 Kisha akawaamuru na kuwaambia: “Mimi ninakusanywa kwa watu wangu.+ Nizikeni pamoja na baba zangu katika pango lililo katika shamba la Efroni Mhiti,+ 30 katika pango lililo katika shamba la Makpela mbele ya Mamre katika nchi ya Kanaani, shamba ambalo Abrahamu alinunua kutoka kwa Efroni Mhiti awe na mahali pa kuzikia.+ 31 Huko walimzika Abrahamu na Sara mke wake.+ Huko walimzika Isaka na Rebeka mke wake,+ na huko nilimzika Lea. 32 Shamba lililonunuliwa na pango lililo ndani yake lilitoka kwa wana wa Hethi.”+

33 Basi Yakobo akamaliza kuwapa wanawe amri. Kisha akaiweka miguu yake pamoja juu ya kitanda, akakata pumzi, akakusanywa kwa watu wake.+

50 Ndipo Yosefu akauangukia uso wa baba yake,+ akamlilia na kumbusu.+ 2 Kisha Yosefu akawaamuru watumishi wake, matabibu, wampake baba yake dawa ya kumfanya asioze.+ Basi wakampaka Israeli dawa ya kumfanya asioze, 3 nao wakatumia siku 40 kamili kwa ajili yake, kwa maana hiyo ndiyo hesabu ya siku ambazo kwa desturi wao hutumia kupaka dawa ya kumfanya mtu asioze, nao Wamisri wakaendelea kumlilia siku 70.+

4 Mwishowe siku za kumlilia zikapita, na Yosefu akawaambia watu wa nyumba ya Farao, akisema: “Ikiwa, sasa, nimepata kibali machoni penu,+ tafadhali, nendeni mkaseme masikioni mwa Farao, na kumwambia, 5 ‘Baba yangu aliniapisha,+ akisema: “Tazama! Ninakufa.+ Katika kaburi ambalo nimechimba mwenyewe katika nchi ya Kanaani+ ndipo utakaponizika.”+ Na sasa, tafadhali, niruhusu niende huko, nikamzike baba yangu, kisha nitarudi.’” 6 Basi Farao akasema: “Nenda ukamzike baba yako kama alivyokuapisha.”+

7 Kwa hiyo Yosefu akaenda kumzika baba yake, na watumishi wote wa Farao, wanaume wazee+ wa nyumba yake na wanaume wote wazee wa nchi ya Misri, wakapanda kwenda pamoja naye, 8 na watu wote wa nyumba ya Yosefu na ndugu zake na nyumba ya baba yake.+ Waliacha tu katika nchi ya Gosheni watoto wao wadogo na makundi yao na mifugo yao. 9 Pia magari+ na wapanda-farasi walienda pamoja naye, nayo kambi ikawa na idadi kubwa sana. 10 Kisha wakafika kwenye uwanja wa kupuria+ wa Atadi, ulio katika eneo la Yordani,+ na huko wakaomboleza maombolezo makuu sana na kulia sana, naye akafanya desturi za kuomboleza kwa ajili ya baba yake kwa siku saba.+ 11 Nao wakaaji wa nchi hiyo, Wakanaani, wakaona desturi za kuomboleza katika uwanja wa kupuria wa Atadi, nao wakasema: “Haya ni maombolezo makuu ya Wamisri!” Ndiyo sababu mahali hapo paliitwa Abel-misraimu, palipo katika eneo la Yordani.+

12 Nao wanawe wakamfanyia kama vile tu alivyokuwa amewaamuru.+ 13 Kwa hiyo wanawe wakampeleka mpaka nchi ya Kanaani na kumzika katika pango la shamba la Makpela, shamba ambalo Abrahamu alikuwa amenunua kutoka kwa Efroni Mhiti mbele ya Mamre+ ili awe na mahali pa kuzikia. 14 Baada ya kumzika baba yake, Yosefu akarudi Misri, yeye na ndugu zake na wale wote waliokwenda pamoja naye kumzika baba yake.

15 Ndugu za Yosefu walipoona kwamba baba yao amekufa, wakaanza kusema: “Huenda ikawa Yosefu anatuwekea uadui+ naye hakika atatulipiza kwa sababu ya uovu wote ambao tumemtendea.”+ 16 Basi wakamjulisha Yosefu amri kwa maneno haya: “Baba yako alitoa amri hii kabla ya kifo chake, akisema, 17 ‘Mtamwambia Yosefu hivi: “Tafadhali, nakuomba, usamehe+ maasi ya ndugu zako na dhambi yao kwa kuwa wamekutendea uovu.”’+ Na tafadhali sasa, usamehe maasi ya watumishi wa Mungu wa baba yako.”+ Naye Yosefu akalia waliposema naye. 18 Halafu ndugu zake pia wakaja na kuanguka chini mbele yake. Wakamwambia: “Tazama, sisi ni kama watumwa kwako!”+ 19 Ndipo Yosefu akawaambia: “Msiogope, kwa maana je, mimi niko mahali pa Mungu?+ 20 Kwa upande wenu, ninyi mlikuwa na uovu akilini mwenu kunielekea mimi. Mungu alikuwa na wema akilini kwa kusudi la kutenda kama ilivyo leo hii ili kuhifadhi hai watu wengi.+ 21 Kwa hiyo sasa msiogope. Mimi nitaendelea kuwapa chakula ninyi na watoto wenu wadogo.”+ Basi akawafariji na kusema nao kwa kuwatuliza.

22 Na Yosefu akaendelea kukaa Misri, yeye na nyumba ya baba yake; na Yosefu akaishi miaka mia moja na kumi. 23 Na Yosefu akapata kuona wana wa Efraimu wa kizazi cha tatu,+ pia wana wa Makiri,+ mwana wa Manase. Walizaliwa juu ya magoti ya Yosefu.+ 24 Mwishowe Yosefu akawaambia ndugu zake: “Ninakufa; lakini Mungu hatakosa kuwaelekezea fikira zake,+ naye kwa hakika atawatoa katika nchi hii na kuwapeleka mpaka nchi ambayo aliwaapia Abrahamu, Isaka na Yakobo.”+ 25 Basi Yosefu akawaapisha wana wa Israeli, akisema: “Mungu hatakosa kuwaelekezea fikira zake. Kwa hiyo mwichukue mifupa yangu kutoka huku.”+ 26 Kisha Yosefu akafa akiwa na umri wa miaka mia moja na kumi; nao wakampaka dawa ya kumfanya asioze,+ naye akatiwa ndani ya sanduku huko Misri.

[Maelezo ya chini]

Sheoli. Tazama Nyongeza 4.

Sheoli. Tazama Nyongeza 4.

Sheoli. Tazama Nyongeza 4.

Sheoli. Tazama Nyongeza 4.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki