Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • bi12 Matendo 1:1-28:31
  • Matendo ya Mitume

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Matendo ya Mitume
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Matendo ya Mitume

Matendo ya Mitume

1 Lile simulizi la kwanza, Ee Theofilo,+ nilitunga juu ya mambo yote ambayo Yesu alianza kufanya na pia kufundisha,+ 2 mpaka siku aliyochukuliwa juu,+ alipokuwa ametoa amri kupitia roho takatifu kwa mitume aliowachagua.+ 3 Kwa uthibitisho mwingi ulio hakika, alijionyesha kwa hawa pia akiwa hai alipokuwa ameteseka,+ nao wakamwona kwa siku 40 na kusema juu ya ufalme wa Mungu.+ 4 Naye alipokuwa akikutana pamoja nao aliwapa maagizo haya: “Msiondoke Yerusalemu,+ bali endeleeni kungojea kile ambacho Baba ameahidi,+ ambacho mlisikia juu yake kutoka kwangu; 5 kwa sababu Yohana, kwa kweli, alibatiza kwa maji, lakini ninyi mtabatizwa kwa roho takatifu+ siku chache baadaye.”

6 Basi, walipokuwa wamekusanyika, wakaanza kumuuliza: “Bwana, je, unarudishia Israeli ufalme+ wakati huu?” 7 Akawaambia: “Si juu yenu kujua nyakati au majira+ ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe;+ 8 lakini mtapokea nguvu+ wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi+ wangu katika Yerusalemu+ na pia katika Yudea yote na Samaria+ na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”+ 9 Na alipokuwa amesema mambo hayo, huku walipokuwa wakitazama, akainuliwa+ na wingu likamchukua juu kutoka machoni pao.+ 10 Nao walipokuwa wakitazama angani alipokuwa ameondoka na kwenda,+ pia, tazama! wanaume wawili wenye mavazi meupe+ wakasimama kando yao, 11 nao wakasema: “Wanaume wa Galilaya, kwa nini mnasimama mkitazama angani? Yesu huyu aliyepokewa juu angani kutoka kwenu atakuja vivyo hivyo+ kama vile ambavyo mmemwona akienda angani.”

12 Ndipo wakarudi+ Yerusalemu kutoka katika mlima unaoitwa Mlima wa Mizeituni, ulio karibu na Yerusalemu, ukiwa ni umbali wa safari ya siku ya sabato.+ 13 Kwa hiyo, walipokuwa wameingia, wakapanda na kuingia katika chumba cha juu,+ ambamo walikuwa wakikaa, Petro vilevile Yohana na Yakobo na Andrea, Filipo na Tomasi, Bartholomayo na Mathayo, Yakobo mwana wa Alfayo na Simoni mwenye bidii, na Yuda mwana wa Yakobo.+ 14 Kwa umoja wote hawa walikuwa wakidumu katika sala,+ pamoja na wanawake+ fulani na Maria mama ya Yesu na pamoja na ndugu zake.+

15 Sasa katika siku hizo Petro akasimama katikati ya akina ndugu na kusema (watu wote pamoja katika ule umati walikuwa karibu 120): 16 “Wanaume, akina ndugu, ilikuwa lazima andiko litimizwe,+ ambalo roho takatifu+ ilisema kimbele kwa kinywa cha Daudi kumhusu Yuda,+ aliyekuwa kiongozi kwa wale waliomkamata Yesu,+ 17 kwa sababu alikuwa amehesabiwa kati yetu+ naye alipata fungu katika huduma hii.+ 18 (Kwa hiyo, mtu huyo alinunua+ shamba kwa mshahara wa ukosefu wa uadilifu,+ akaanguka kichwa kwanza+ akapasuka kwa kelele katikati na matumbo yake yote yakamwagika nje. 19 Pia ikajulikana kwa wakaaji wote wa Yerusalemu, hivi kwamba shamba hilo likaitwa katika lugha yao Akeldama, yaani, Shamba la Damu.) 20 Kwa maana imeandikwa katika kitabu cha Zaburi, ‘Makao yake yawe na ukiwa, na pasiwe na mkaaji humo,’+ na, ‘Cheo chake cha uangalizi mtu mwingine na akichukue.’+ 21 Kwa hiyo ni lazima kwamba kati ya wanaume waliokusanyika pamoja nasi wakati wote ambao Bwana Yesu aliingia na kutoka kati yetu,+ 22 kuanzia na ubatizo wake uliofanywa na Yohana+ mpaka siku aliyopokewa juu kutoka kwetu,+ mmoja wa watu hao anapaswa kuwa shahidi pamoja nasi juu ya ufufuo wake.”+

23 Kwa hiyo wakasimamisha wawili, Yosefu anayeitwa Barsaba, aliyeitwa pia Yusto, na Mathia. 24 Nao wakasali na kusema: “Wewe, Ee Yehova, ambaye unajua mioyo ya wote,+ onyesha ni nani kati ya watu hawa wawili ambaye umemchagua, 25 achukue mahali pa huduma na utume+ huu, ambao kutoka kwake Yuda alikengeuka ili kwenda mahali pake mwenyewe.” 26 Kwa hiyo wakawapigia kura,+ na kura ikamwangukia Mathia; naye akahesabiwa pamoja na wale mitume kumi na mmoja.+

2 Basi siku ya sherehe ya Pentekoste+ ilipokuwa ikiendelea walikuwa wote pamoja mahali pale pale, 2 na ghafula kukatokea kutoka mbinguni kelele kama ile ya upepo wenye nguvu unaovuma, nao ukaijaza nyumba yote ambamo walikuwa wameketi.+ 3 Nao wakaona ndimi kama za moto,+ nazo zikagawanyika huku na huku, na mmoja ukaketi juu ya kila mmoja wao, 4 nao wote wakajazwa roho takatifu+ wakaanza kusema katika lugha+ tofauti, kama vile roho ilivyokuwa ikiwawezesha kusema.

5 Ikawa kwamba, kulikuwa na Wayahudi+ wakikaa katika Yerusalemu, watu wenye kumheshimu Mungu,+ kutoka kila taifa kati ya yale yaliyo chini ya mbingu. 6 Kwa hiyo, mvumo huo ulipotokea, umati ukaja pamoja nao ukashikwa na bumbuazi, kwa sababu kila mmoja aliwasikia wakisema katika lugha yake mwenyewe. 7 Kwa kweli, walishangaa na kuanza kustaajabu na kusema: “Tazama, wote hawa wanaosema ni Wagalilaya,+ sivyo? 8 Hata hivyo, imewezekanaje kwamba sisi, kila mmoja wetu, tunasikia lugha yake mwenyewe tuliyozaliwa nayo? 9 Waparthi na Wamedi+ na Waelami,+ na wakaaji wa Mesopotamia, na Yudea+ na Kapadokia,+ Ponto+ na wilaya ya Asia,+ 10 na Frigia+ na Pamfilia,+ Misri, na sehemu za Libya, ambayo ni kuelekea Kirene, na wakaaji wa muda wa kutoka Roma, Wayahudi na pia wageuzwa-imani,+ 11 Wakrete+ na Waarabu,+ tunawasikia wakisema katika lugha zetu juu ya mambo makuu ya Mungu.” 12 Ndiyo, wote wakashangaa na kustaajabu, wakiambiana: “Jambo hili linamaanisha nini?” 13 Hata hivyo, watu tofauti waliwadhihaki na kuanza kusema: “Wamejaa divai tamu.”+

14 Lakini Petro akasimama pamoja na wale kumi na mmoja+ na kupaaza sauti yake na kuwaambia hivi: “Watu wa Yudea nanyi nyote wakaaji wa Yerusalemu,+ acheni hili lijulikane kwenu nanyi tegeni sikio msikie maneno yangu. 15 Kwa kweli, watu hawa hawakulewa,+ kama mnavyofikiri, kwa maana ni saa tatu ya mchana. 16 Badala yake, hili ndilo lililosemwa kupitia nabii Yoeli, 17 ‘ “Na katika siku za mwisho,” Mungu asema, “Nitaimimina sehemu ya roho yangu+ juu ya kila namna ya mwili, nao wana wenu na binti zenu watatoa unabii nao wanaume wenu vijana wataona maono na wazee wenu wataota ndoto;+ 18 na hata juu ya watumwa wangu na juu ya wajakazi wangu nitaimimina sehemu ya roho yangu katika siku hizo, nao watatoa unabii.+ 19 Nami nitatoa maajabu mbinguni juu na ishara duniani chini, damu na moto na ukungu wa moshi;+ 20 jua+ litageuzwa kuwa giza na mwezi kuwa damu kabla ya kufika kwa ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye fahari.+ 21 Na kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.” ’+

22 “Watu wa Israeli, sikieni maneno haya: Yesu Mnazareti,+ mwanamume aliyeonyeshwa hadharani na Mungu kwenu kupitia kazi zenye nguvu+ na mambo ya ajabu na ishara ambazo Mungu alifanya kupitia kwake katikati yenu,+ kama vile ninyi wenyewe mnavyojua, 23 mwanamume huyu, kama aliyetolewa kwa shauri lililoamuliwa na kwa ujuzi wa kimbele wa Mungu,+ mlimfunga kwenye mti kwa mkono wa waasi-sheria na kumwondolea mbali.+ 24 Lakini Mungu alimfufua+ kwa kuyafungua maumivu makali ya kifo,+ kwa sababu haikuwezekana kiendelee kumshika.+ 25 Kwa maana Daudi anasema juu yake, ‘Yehova alikuwa mbele ya macho yangu daima; kwa sababu yuko upande wa mkono wangu wa kuume ili nisipate kutikiswa kamwe.+ 26 Kwa ajili ya hilo moyo wangu ulichangamka na ulimi wangu ukashangilia sana. Zaidi ya hayo, hata mwili wangu utakaa katika tumaini;+ 27 kwa sababu hutaiacha nafsi yangu katika Kaburi,* wala hutamruhusu mshikamanifu wako aone uharibifu.+ 28 Umefanya njia za uzima zijulikane kwangu, utanijaza uchangamfu mwingi kwa uso wako.’+

29 “Wanaume, akina ndugu, inaruhusika kusema nanyi kwa uhuru wa kusema juu ya Daudi yule kichwa cha familia, kwamba alikufa+ na pia akazikwa na kaburi lake liko katikati yetu mpaka leo hii. 30 Kwa hiyo, kwa sababu alikuwa nabii na alijua kwamba Mungu alikuwa amemwapia kwa kiapo kwamba angemketisha mmoja kutoka kati ya uzao wa viuno vyake juu ya kiti chake cha ufalme,+ 31 aliona kimbele na kusema kuhusu ufufuo wa Kristo, kwamba hakuachwa katika Kaburi* wala mwili wake haukuona uharibifu.+ 32 Yesu huyo Mungu alimfufua, uhakika ambao sisi sote ni mashahidi.+ 33 Kwa hiyo kwa sababu aliinuliwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu+ na kupokea roho takatifu iliyoahidiwa kutoka kwa Baba,+ amemimina hiki ambacho ninyi mnakiona na kukisikia. 34 Kwa kweli Daudi hakupanda mbinguni,+ bali yeye mwenyewe anasema, ‘Yehova alimwambia Bwana wangu: “Keti kwenye mkono wangu wa kuume,+ 35 mpaka niwaweke adui zako kuwa kiti cha miguu yako.” ’+ 36 Kwa hiyo acha nyumba yote ya Israeli ijue kwa hakika kwamba Mungu alimfanya Bwana+ na pia Kristo, Yesu huyu ambaye ninyi mlimtundika mtini.”+

37 Basi waliposikia hilo walichomwa moyoni,+ nao wakamwambia Petro na wale mitume wengine: “Wanaume, akina ndugu, tufanye nini?”+ 38 Petro akawaambia: “Tubuni,+ na acheni kila mmoja wenu abatizwe+ katika jina+ la Yesu Kristo kwa msamaha+ wa dhambi zenu, nanyi mtapokea zawadi ya bure+ ya roho takatifu. 39 Kwa maana ahadi+ ni kwenu na kwa watoto wenu na kwa wale wote walio mbali,+ wengi kadiri ambayo Yehova Mungu wetu huenda akawaita kwake.”+ 40 Na kwa maneno mengine mengi akatoa ushahidi kamili na kuendelea kuwahimiza, akisema: “Okoleweni kutoka katika kizazi hiki kilicho kombo.”+ 41 Kwa hiyo wale waliokubali neno lake kwa ukunjufu wa moyo wakabatizwa,+ na katika siku hiyo nafsi karibu elfu tatu zikaongezwa.+ 42 Nao wakaendelea kujitoa wenyewe kwa fundisho la mitume na kushirikiana,+ katika kula milo+ na katika sala.+

43 Kwa kweli, woga ukaanza kuwa juu ya kila nafsi, na mambo mengi ya ajabu na ishara nyingi zikaanza kutukia kupitia mitume.+ 44 Wale wote waliopata kuwa waamini walikuwa pamoja katika kuwa na mambo yote kwa ushirika,+ 45 nao wakaanza kuuza miliki na mali zao+ na kuwagawia wote mapato hayo, kulingana na vile yeyote alivyokuwa na uhitaji.+ 46 Na siku baada ya siku walikuwa wakihudhuria daima kwenye hekalu kwa umoja,+ nao walikula milo yao katika nyumba za faragha na kushiriki chakula kwa shangwe+ kuu na weupe wa moyo, 47 wakimsifu Mungu na kupata kibali kwa watu wote.+ Wakati uleule Yehova akaendelea kuongezea+ kwao kila siku wale waliokuwa wakiokolewa.+

3 Basi Petro na Yohana walikuwa wakipanda kwenda hekaluni kwa ajili ya saa ya sala, saa tisa,+ 2 na mwanamume fulani aliyekuwa kilema tangu alipokuwa katika tumbo la uzazi la mama yake+ alikuwa akibebwa, nao walikuwa wakimweka kila siku karibu na mlango wa hekalu ulioitwa Mzuri,+ ili kuomba zawadi za rehema kutoka kwa wale waliokuwa wakiingia katika hekalu.+ 3 Alipowaona Petro na Yohana wakiwa karibu kuingia ndani ya hekalu akaanza kuomba apate zawadi za rehema.+ 4 Lakini Petro, pamoja na Yohana, wakamtazama+ na kusema: “Tuangalie sisi.” 5 Kwa hiyo akawaangalia, akitarajia kupata kitu fulani kutoka kwao. 6 Hata hivyo, Petro akasema: “Fedha na dhahabu sina, lakini kile nilicho nacho ndicho ninachokupa:+ Katika jina la Yesu Kristo Mnazareti,+ tembea!”+ 7 Ndipo akamshika mkono wa kuume na kumwinua.+ Papo hapo nyayo za miguu yake na vifundo vya miguu yake vikafanywa imara;+ 8 naye akaruka juu,+ akasimama na kuanza kutembea, kisha akaingia pamoja nao katika hekalu,+ akitembea na kuruka-ruka na kumsifu Mungu. 9 Na watu wote+ wakamwona akitembea na kumsifu Mungu. 10 Zaidi ya hayo, wakaanza kumtambua, kwamba huyu ndiye mtu aliyekuwa akiketi kwa ajili ya zawadi za rehema penye Lango Zuri+ la hekalu, nao wakajawa na mshangao na shangwe+ kwa sababu ya jambo lililokuwa limetukia kwake.

11 Basi, kwa kuwa mtu huyo alikuwa akiwashikilia Petro na Yohana, watu wote waliwakimbilia pamoja kwenye eneo lililoitwa mistari ya nguzo za Sulemani,+ wakiwa wamepotewa na akili kwa sababu ya mshangao. 12 Petro alipoona jambo hilo, akawaambia watu hao: “Watu wa Israeli, kwa nini mnastaajabu juu ya hili, au kwa nini mnatutazama kana kwamba tumemfanya atembee kwa nguvu za kibinafsi au kwa ujitoaji-kimungu?+ 13 Mungu wa Abrahamu na wa Isaka na wa Yakobo,+ Mungu wa mababu zetu, amemtukuza+ Mtumishi+ wake, Yesu, ambaye ninyi mlimpeleka+ na kumkana mbele ya uso wa Pilato, alipokuwa ameamua kumfungua.+ 14 Ndiyo, ninyi mlimkana huyo aliye mtakatifu na mwadilifu,+ nanyi mkaomba mpewe kwa hiari mwanamume, muuaji,+ 15 lakini mlimuua Wakili Mkuu wa uzima.+ Lakini Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, uhakika ambao sisi ni mashahidi+ wake. 16 Kwa sababu hiyo, kwa imani yetu katika jina lake, jina lake limemfanya awe mwenye nguvu mtu huyu ambaye mnamwona na kumjua, na imani kupitia kwake imempa mtu huyu afya hii kamili mbele ya macho yenu nyote. 17 Na sasa, akina ndugu, ninajua kwamba mlitenda kwa kutojua,+ kama vile watawala+ wenu pia walivyotenda. 18 Lakini katika njia hiyo Mungu ametimiza mambo aliyotangaza kimbele kupitia kinywa cha manabii wote, kwamba Kristo wake angeteseka.+

19 “Kwa hiyo, tubuni+ na mgeuke+ ili dhambi zenu zipate kufutwa,+ ili majira ya kuburudisha+ yapate kuja kutoka kwa uso wa Yehova 20 na kwamba apate kumtuma Kristo aliyewekwa rasmi kwa ajili yenu, Yesu, 21 ambaye mbingu, kwa kweli,+ lazima imweke ndani yake mpaka nyakati za kurudishwa+ kwa mambo yote ambayo Mungu alisema kupitia kinywa cha manabii+ wake watakatifu wa nyakati za kale. 22 Kwa kweli, Musa alisema, ‘Yehova Mungu atawainulia kutoka kati ya ndugu zenu nabii kama mimi.+ Msikilizeni huyo kulingana na mambo yote anayowaambia ninyi.+ 23 Kwa kweli, nafsi yoyote isiyomsikiliza Nabii huyo itaangamizwa kutoka kati ya watu.’+ 24 Na kwa kweli, manabii wote tangu Samweli na kuendelea na wale waliofuata, wengi kadiri ambavyo wamesema, wamezitangaza waziwazi pia siku hizi.+ 25 Ninyi ndio wana+ wa manabii na wa agano ambalo Mungu aliagana pamoja na mababu zenu, akimwambia Abrahamu, ‘Na katika uzao wako familia zote za dunia zitabarikiwa.’+ 26 Baada ya kumwinua Mtumishi wake, Mungu alimtuma kwenu kwanza+ ili kuwabariki ninyi kwa kugeuzia mbali kila mmoja kutoka kwenye matendo yenu maovu.”

4 Sasa hao wawili walipokuwa wakisema na watu, wakuu wa makuhani na kapteni wa hekalu+ na Masadukayo+ wakawajia, 2 wakiwa wameudhika kwa sababu walikuwa wakiwafundisha watu na walikuwa wakiutangaza waziwazi ufufuo kutoka kwa wafu kwa kisa cha Yesu;+ 3 nao wakawashika na kuwaweka katika kizuizi mpaka siku iliyofuata,+ kwa maana tayari ilikuwa jioni. 4 Hata hivyo, wengi kati ya wale waliokuwa wamesikiliza maneno hayo wakaamini,+ na hesabu ya wanaume ikawa karibu elfu tano.+

5 Siku iliyofuata kukawa na mkutano wa watawala wao na wanaume wazee na waandishi katika Yerusalemu+ 6 (pia Anasi+ mkuu wa makuhani na Kayafa+ na Yohana na Aleksanda na wengi waliokuwa watu wa jamaa ya huyo mkuu wa makuhani), 7 nao wakawasimamisha katikati yao na kuanza kuuliza: “Mlifanya jambo hilo kwa nguvu gani au katika jina la nani?”+ 8 Ndipo Petro, akiwa amejazwa roho takatifu,+ akawaambia:

“Watawala wa watu na wanaume wazee, 9 ikiwa leo sisi tunahojiwa, juu ya msingi wa tendo jema kwa mtu mwenye kuugua,+ kuhusu ni nani amemponya mtu huyu, 10 acheni ijulikane kwenu nyote na kwa watu wote wa Israeli, kwamba katika jina la Yesu Kristo Mnazareti,+ ambaye mlimtundika mtini+ lakini ambaye Mungu alimfufua kutoka kwa wafu,+ kupitia kwake, mtu huyu anasimama hapa akiwa na afya mbele yenu. 11 Hilo ndilo ‘jiwe ambalo ninyi wajenzi mlilitendea kana kwamba si la maana ambalo limekuwa jiwe kuu la pembeni.’+ 12 Zaidi ya hayo, hakuna wokovu katika mwingine yeyote, kwa maana hakuna jina+ lingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu ambalo kupitia hilo lazima sisi tupate kuokolewa.”+

13 Sasa walipoona maneno ya waziwazi ya Petro na Yohana, na kufahamu kwamba walikuwa watu wasio na elimu na wa kawaida tu,+ wakaanza kustaajabu. Nao wakaanza kutambua juu yao kwamba walikuwa pamoja na Yesu;+ 14 nao walipokuwa wakitazama mtu aliyekuwa ameponywa akiwa amesimama pamoja nao,+ hawakuwa na jambo la kukanusha.+ 15 Kwa hiyo wakawaamuru waende nje ya jumba la Sanhedrini, nao wakaanza kushauriana, 16 wakisema: “Tutafanya nini na watu hawa?+ Kwa sababu, kwa kweli, ishara kuu imetukia kupitia kwao, ambayo ni wazi kwa wakaaji wote wa Yerusalemu;+ nasi hatuwezi kuikana. 17 Hata hivyo, ili isipate kusambazwa zaidi kotekote kati ya watu, acheni tuwaambie kwa vitisho wasiseme tena kamwe na mtu yeyote juu ya msingi wa jina hilo.”+

18 Ndipo wakawaita na kuwaamuru wasiseme wala kufundisha popote juu ya msingi wa jina la Yesu. 19 Lakini Petro na Yohana wakajibu wakawaambia: “Kama ni jambo la uadilifu mbele za macho ya Mungu kuwasikiliza ninyi badala ya Mungu, hukumuni ninyi wenyewe. 20 Lakini sisi hatuwezi kuacha kusema juu ya mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.”+ 21 Kwa hiyo, walipokuwa wamewatisha zaidi, wakawafungua, kwa kuwa hawakupata msingi wowote wa kuwaadhibu na kwa sababu ya watu,+ kwa sababu wote walikuwa wakimtukuza Mungu juu ya jambo lililokuwa limetukia; 22 kwa maana mtu ambaye ishara hiyo ya kuponywa ilikuwa imetokea juu yake alikuwa na umri wa zaidi ya miaka 40.

23 Baada ya kufunguliwa wakaenda kwa watu wao+ wenyewe na kuwaeleza mambo ambayo wakuu wa makuhani na wanaume wazee walikuwa wamewaambia. 24 Waliposikia hayo wakampaazia Mungu+ sauti zao kwa umoja na kusema:

“Bwana Mwenye Enzi Kuu,+ wewe Ndiye uliyefanya mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo,+ 25 na ambaye kupitia roho takatifu ulisema kwa kinywa cha babu yetu Daudi,+ mtumishi wako, ‘Kwa nini mataifa yakawa yenye fujo na vikundi vya watu vikatafakari juu ya mambo matupu?+ 26 Wafalme wa dunia walichukua msimamo wao nao watawala wakajikusanya pamoja kama mtu mmoja dhidi ya Yehova na dhidi ya mtiwa-mafuta wake.’+ 27 Ijapokuwa hivyo, Herode na pia Pontio Pilato+ pamoja na watu wa mataifa na pamoja na vikundi vya watu wa Israeli kwa kweli walikusanyika pamoja katika jiji hili dhidi ya mtumishi wako mtakatifu+ Yesu, ambaye ulimtia mafuta,+ 28 ili afanye mambo ambayo mkono wako na shauri viliagiza kimbele yatukie.+ 29 Na sasa, Yehova, viangalie vitisho vyao,+ na kuwawezesha watumwa wako kuendelea kusema neno lako kwa ujasiri wote,+ 30 huku ukiunyoosha mkono wako ili kuponya na huku ishara+ nyingi na mambo ya ajabu yakitukia kupitia jina+ la mtumishi+ wako mtakatifu Yesu.”

31 Nao walipokuwa wameomba dua, mahali hapo walipokuwa wamekusanyika pamoja pakatikiswa;+ nao wote wakajazwa roho takatifu+ na wakawa wakisema neno la Mungu kwa ujasiri.+

32 Zaidi ya hayo, umati wa waliokuwa wameamini ulikuwa na moyo na nafsi moja,+ na hakuna hata mmoja aliyekuwa akisema kwamba chochote kati ya vitu vilivyokuwa mali yake kilikuwa chake mwenyewe; bali walikuwa na vitu vyote kwa ushirika.+ 33 Pia, wakiwa na nguvu nyingi mitume wakaendelea kutoa ushahidi kuhusu ufufuo wa Bwana Yesu;+ na fadhili zisizostahiliwa kwa kadiri kubwa zilikuwa juu yao wote. 34 Kwa kweli, hapakuwa hata mmoja mwenye uhitaji kati yao;+ kwa maana wale wote waliokuwa na mashamba au nyumba walikuwa wakiviuza na kuleta thamani za vitu vilivyouzwa 35 nao walikuwa wakiziweka miguuni pa mitume.+ Na kila mmoja alikuwa akigawiwa,+ kulingana na uhitaji wake. 36 Kwa hiyo Yosefu, ambaye mitume walikuwa wakimwita Barnaba,+ jina ambalo linapotafsiriwa linamaanisha Mwana wa Faraja, Mlawi, mzaliwa wa Kipro, 37 akiwa na sehemu ya shamba, akaiuza na kuzileta pesa na kuziweka miguuni pa mitume.+

5 Hata hivyo, mwanamume fulani, aliyeitwa Anania, pamoja na Safira mke wake, aliuza mali 2 na kujiwekea kwa siri kiasi fulani, mke wake pia akiwa anajua jambo hilo, naye akaleta sehemu fulani tu na kuiweka miguuni pa mitume.+ 3 Lakini Petro akasema: “Anania, kwa nini Shetani+ amekupa ujasiri wa kuidanganya+ roho takatifu+ na kujiwekea kwa siri kiasi fulani cha bei ya shamba? 4 Kabla ya kuuza je, haikuwa mali yako, na baada ya kuuza je, haikuendelea kuwa mikononi mwako? Kwa nini ukakusudia tendo kama hili katika moyo wako? Umedanganya,+ si wanadamu, bali Mungu.”+ 5 Aliposikia maneno hayo Anania akaanguka chini akakata pumzi.+ Na wote waliosikia juu ya hilo wakaogopa+ sana. 6 Lakini vijana wakasimama, wakamfunga kwa vitambaa,+ wakamtoa nje, wakamzika.

7 Sasa baada ya muda wa karibu saa tatu mke wake akaingia, bila kujua lililokuwa limetukia. 8 Petro akamwambia: “Niambie, je, ninyi wawili mliliuza shamba kwa kiasi hicho?” Akasema: “Ndiyo, kwa kiasi hicho.” 9 Kwa hiyo Petro akamwambia: “Kwa nini mlikubaliana kati yenu wawili kuijaribu+ roho ya Yehova? Tazama! Miguu ya wale waliomzika mume wako ipo mlangoni, nao watakubeba na kukutoa nje.” 10 Papo hapo akaanguka chini miguuni pake akakata pumzi.+ Wale vijana walipoingia wakamkuta amekufa, nao wakamtoa nje wakamzika kando ya mume wake. 11 Kwa sababu hiyo kutaniko lote na wote waliosikia juu ya mambo haya wakaogopa sana.

12 Zaidi ya hayo, kupitia mikono ya mitume ishara nyingi na mambo ya ajabu yakaendelea kutukia kati ya watu;+ nao wote walikuwa kwa umoja katika eneo lenye mistari ya nguzo za Sulemani.+ 13 Kweli, hakuna hata mmoja kati ya wale wengine aliyekuwa na moyo wa kujiunga nao;+ hata hivyo, watu walikuwa wakiwahimidi.+ 14 Zaidi ya hayo, waliomwamini Bwana wakaendelea kuongezeka, umati wa wanaume na pia wa wanawake;+ 15 hivi kwamba wakawaleta wagonjwa nje hata katika zile njia pana na kuwalaza huko juu ya vitanda na machela, ili, wakati Petro anapopita hapo, angalau kivuli chake kipate kumwangukia mtu fulani kati yao.+ 16 Pia, umati kutoka kwenye majiji yanayozunguka Yerusalemu ukazidi kuja pamoja, ukiwa umewabeba wagonjwa na wale wenye kutaabika wakiwa na roho wachafu, nao wote wakawa wakiponywa.

17 Lakini kuhani mkuu na wote waliokuwa pamoja naye, ile madhehebu ya Masadukayo iliyokuwako wakati huo, wakasimama na kujawa na wivu,+ 18 nao wakawashika mitume na kuwaweka katika kizuizi cha watu wote.+ 19 Lakini wakati wa usiku malaika+ wa Yehova akaifungua milango ya gereza,+ akawatoa nje na kusema: 20 “Nendeni, na, mkiisha kusimama katika hekalu, semeni na watu maneno yote juu ya maisha haya.”+ 21 Baada ya kusikia hilo, wakaingia hekaluni wakati wa mapambazuko na kuanza kufundisha.

Basi kuhani mkuu na wale walio pamoja naye walipofika, wakaita pamoja Sanhedrini na kusanyiko lote la wanaume wazee wa wana wa Israeli,+ nao wakawatuma watu kwenye jela ili waletwe. 22 Lakini wale maofisa walipofika huko hawakuwakuta gerezani. Kwa hiyo wakarudi na kuwaeleza, 23 wakisema: “Tuliikuta jela imefungwa ikiwa na usalama wote na walinzi wakiwa wamesimama kwenye milango, lakini tulipofungua hatukumkuta yeyote ndani.” 24 Basi, wakati kapteni wa hekalu na tena wakuu wa makuhani waliposikia maneno hayo, wakafadhaishwa sana na mambo hayo wasijue mwisho wa jambo hilo ungekuwa nini.+ 25 Lakini mtu fulani akafika na kuwaambia: “Tazameni! Wale watu mliowaweka gerezani wako hekaluni, wakiwa wamesimama na kuwafundisha watu.”+ 26 Ndipo kapteni akaenda zake pamoja na maofisa wake na kuwaleta, lakini bila kutumia jeuri, maana waliogopa+ kupigwa na watu kwa mawe.

27 Kwa hiyo wakawaleta na kuwasimamisha katika jumba la Sanhedrini. Na kuhani mkuu akawauliza 28 na kusema: “Hakika tuliwaagiza+ msiendelee kufundisha juu ya msingi wa jina hili, na bado, tazameni! mmejaza Yerusalemu fundisho lenu,+ nanyi mnaazimia kuileta damu+ ya mtu huyu juu yetu.” 29 Petro na wale mitume wengine wakajibu wakasema: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.+ 30 Mungu wa mababu zetu alimfufua+ Yesu, ambaye ninyi mlimuua, kwa kumtundika mtini.+ 31 Mungu alimwinua huyo kuwa Wakili Mkuu+ na Mwokozi+ kwenye mkono wake wa kuume,+ ili kuwapa Israeli toba+ na msamaha wa dhambi.+ 32 Nasi ni mashahidi wa mambo hayo,+ na pia roho takatifu,+ ambayo Mungu amewapa wale wanaomtii yeye akiwa mtawala.”

33 Waliposikia hayo, wakahisi wamechomwa sana nao wakataka kuwaangamiza.+ 34 Lakini mtu fulani akasimama katika Sanhedrini, Farisayo anayeitwa Gamalieli,+ mwalimu wa Sheria mwenye kuheshimiwa na watu wote, akaamuru watu hao watolewe nje kwa muda kidogo.+ 35 Naye akawaambia: “Wanaume wa Israeli,+ jiangalieni ninyi wenyewe kuhusu jambo mnalokusudia kuwatendea watu hawa. 36 Kwa mfano, kabla ya siku hizi Theuda alisimama, akisema yeye mwenyewe alikuwa mtu wa maana,+ na wanaume kadhaa, karibu mia nne, wakajiunga na chama chake.+ Lakini aliangamizwa, na wote waliokuwa wakimtii wakatawanywa na kumalizwa. 37 Baada yake Yuda Mgalilaya akainuka katika zile siku za uandikishaji,+ naye akavuta watu wamfuate. Na bado mtu huyo aliangamia, na wale wote waliokuwa wakimtii wakatapanywa kotekote. 38 Na kwa hiyo, chini ya hali zilizopo, ninawaambia ninyi, Msijiingize katika mambo ya watu hawa, bali waacheni; (kwa sababu, ikiwa mpango huu au kazi hii imetoka kwa wanadamu, itaangamizwa;+ 39 lakini ikiwa imetoka kwa Mungu,+ hamtaweza kuwaangamiza;)+ ama sivyo, huenda mkaonwa kuwa kwa kweli mnapigana na Mungu.”+ 40 Ndipo wakamsikiliza, nao wakawaita mitume, wakawapiga viboko,+ na kuwaagiza waache kusema juu ya msingi wa jina la Yesu,+ kisha wakawaacha waende zao.

41 Kwa hiyo, wakatoka mbele ya Sanhedrini, wakishangilia+ kwa sababu walikuwa wamehesabiwa kuwa wenye kustahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake.+ 42 Na kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba+ wakaendelea bila kuacha kufundisha+ na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.+

6 Basi katika siku hizo, wanafunzi walipokuwa wakiongezeka, Wayahudi wenye kusema Kigiriki+ walianza kunung’unika juu ya Wayahudi wenye kusema Kiebrania, kwa sababu wajane wao walikuwa hawaangaliwi katika ugawaji wa kila siku.+ 2 Kwa hiyo wale kumi na wawili wakauita umati wa wanafunzi na kusema: “Si vyema sisi kuliacha neno la Mungu ili kugawa chakula mezani.+ 3 Kwa hiyo, akina ndugu, jitafutieni+ wanaume saba waliothibitishwa kutoka kati yenu, wenye kujaa roho na hekima,+ ili tupate kuwaweka rasmi juu ya kazi hii ya lazima; 4 lakini sisi tutajitoa kwa sala na kwa huduma ya neno.”+ 5 Na jambo hilo lililosemwa likaupendeza umati wote, nao wakamchagua Stefano, mwanamume mwenye kujaa imani na roho takatifu,+ na Filipo+ na Prokoro na Nikanori na Timoni na Parmena na Nikolao, mgeuzwa-imani wa Antiokia; 6 nao wakawaweka mbele ya mitume, na, wakiisha kusali, hao wakaweka mikono+ yao juu yao.

7 Kwa sababu hiyo neno la Mungu likaendelea kukua,+ na hesabu ya wanafunzi ikazidi kuongezeka sana katika Yerusalemu;+ na umati mkubwa wa makuhani+ ukaanza kuitii+ imani.

8 Sasa Stefano, akiwa amejaa neema na nguvu, alikuwa akifanya mambo makubwa ya ajabu na ishara+ kati ya watu. 9 Lakini watu fulani wakasimama kati ya wale waliokuwa wakitoka katika lile lililoitwa Sinagogi la Watu Waliowekwa Huru, na kati ya Wakirene na Waaleksandria+ na kati ya wale wa kutoka Kilikia+ na Asia, ili kubishana na Stefano; 10 na bado hawakuweza kufaulu katika pambano juu ya hekima+ na roho aliyokuwa akisema kwayo.+ 11 Ndipo kwa siri wakashawishi watu kusema:+ “Tumemsikia akisema maneno ya makufuru+ juu ya Musa na Mungu.” 12 Nao wakawachochea watu na wanaume wazee na waandishi, wakamjia ghafula, wakamchukua kwa nguvu na kumpeleka mpaka kwenye Sanhedrini.+ 13 Nao wakatokeza mashahidi wa uwongo,+ waliosema: “Mtu huyu haachi kusema mambo yasiyofaa juu ya mahali hapa patakatifu na juu ya Sheria.+ 14 Kwa mfano, tumemsikia akisema kwamba huyu Yesu Mnazareti atapaangusha chini mahali hapa na kuzibadili desturi ambazo Musa alitukabidhi.”

15 Na wote waliokuwa wameketi katika Sanhedrini walipokuwa wakimkazia macho,+ wakaona kwamba uso wake ulikuwa kama uso wa malaika.+

7 Lakini kuhani mkuu akasema: “Je, mambo haya ndivyo yalivyo?” 2 Akasema: “Wanaume, akina ndugu na akina baba, sikieni. Mungu wa utukufu+ alimtokea babu yetu Abrahamu alipokuwa Mesopotamia, kabla ya kuanza kukaa Harani,+ 3 naye akamwambia, ‘Toka katika nchi yako na kutoka kwa watu wa jamaa yako na uje mpaka katika nchi ambayo nitakuonyesha.’+ 4 Ndipo akatoka nchi ya Wakaldayo na kuanza kukaa Harani. Na kutoka huko, baada ya baba yake kufa,+ Mungu akamfanya abadili makao yake mpaka kwenye nchi hii ambamo ninyi sasa mnakaa.+ 5 Na bado hakumpa urithi wowote ndani yake, hapana, hata upana wa wayo mmoja wa mguu;+ bali aliahidi kumpa hiyo kuwa miliki,+ na uzao wake baada yake,+ alipokuwa bado hana mtoto.+ 6 Zaidi ya hayo, Mungu alisema hivi, kwamba uzao wake ungekuwa wakaaji wageni+ katika nchi ya kigeni+ na watu hao wangewafanya watumwa na kuwatesa kwa miaka mia nne.+ 7 ‘Na taifa ambalo watalitumikia nitalihukumu,’+ Mungu akasema, ‘na baada ya mambo hayo watatoka na kunitolea utumishi mtakatifu mahali hapa.’+

8 “Alimpa pia agano la tohara;+ na kwa hiyo akamzaa Isaka+ na kumtahiri siku ya nane,+ na Isaka akamzaa Yakobo, na Yakobo akawazaa wale vichwa vya familia kumi na wawili.+ 9 Na wale vichwa vya familia wakamwonea Yosefu wivu+ na kumuuza Misri.+ Lakini Mungu alikuwa pamoja naye,+ 10 naye akamkomboa kutoka katika dhiki zake zote na kumpa neema na hekima machoni pa Farao mfalme wa Misri. Naye akamweka aongoze Misri na nyumba yake yote.+ 11 Lakini njaa ikaja juu ya Misri yote na Kanaani, hata dhiki kuu; na mababu zetu hawakuwa wakipata chakula chochote.+ 12 Lakini Yakobo akasikia kulikuwa na vyakula Misri+ naye akawatuma mababu zetu mara ya kwanza.+ 13 Na mara ya pili Yosefu akajulishwa kwa ndugu zake;+ na ukoo wa familia ya Yosefu ukajulishwa kwa Farao.+ 14 Kwa hiyo Yosefu akatuma watu wamwite Yakobo baba yake na jamaa zake wote kutoka hapo,+ wenye kufikia hesabu ya nafsi 75.+ 15 Yakobo akashuka kuingia Misri.+ Naye akafa;+ na pia mababu zetu,+ 16 nao wakahamishwa mpaka Shekemu+ na kulazwa katika kaburi+ ambalo Abrahamu alikuwa amenunua kwa bei fulani kwa fedha kutoka kwa wana wa Hamori katika Shekemu.+

17 “Wakati ulipokuwa ukikaribia kwa ajili ya utimizo wa ahadi ambayo Mungu alikuwa amemtangazia Abrahamu waziwazi, watu wakaongezeka na kuzidi katika Misri,+ 18 mpaka akainuka mfalme tofauti juu ya Misri, ambaye hakujua habari za Yosefu.+ 19 Huyo akatumia hila ya serikali juu ya jamii+ yetu na kulazimisha kimakosa akina baba wawatupe watoto wao wachanga, ili wasihifadhiwe hai.+ 20 Katika wakati huo maalumu Musa akazaliwa,+ naye alikuwa mwenye sura nzuri+ machoni pa Mungu. Naye akanyonyeshwa kwa miezi mitatu nyumbani mwa baba yake. 21 Lakini alipotupwa, binti ya Farao akamwokota na kumlea kama mwana wake mwenyewe.+ 22 Kwa sababu hiyo Musa akafundishwa hekima+ yote ya Wamisri. Kwa kweli, yeye alikuwa mwenye nguvu katika maneno+ na matendo.

23 “Sasa wakati wa mwaka wake wa 40 ulipokuwa ukitimia, wazo likaingia moyoni mwake, awakague ndugu zake, wana wa Israeli.+ 24 Naye alipomwona mtu fulani akitendewa isivyo haki, akamtetea na kulipiza kisasi kwa ajili ya yule mwenye kutendewa vibaya kwa kumpiga na kumuua Mmisri.+ 25 Alikuwa akidhani ndugu zake wangefahamu ya kwamba Mungu alikuwa akiwapa wokovu kwa mkono wake,+ lakini hawakufahamu hilo. 26 Na siku iliyofuata akawatokea walipokuwa wakipigana, naye akajaribu kuwapatanisha tena wawe na amani,+ akisema, ‘Wanaume, ninyi ni ndugu. Kwa nini mnatendeana isivyo haki?’+ 27 Lakini yule aliyekuwa akimtendea jirani yake isivyo haki akamsukuma mbali, akisema, ‘Ni nani aliyekuweka wewe kuwa mtawala na mwamuzi juu yetu?+ 28 Unataka kuniangamiza vile ulivyomwangamiza yule Mmisri jana, sivyo?’+ 29 Kwa maneno hayo Musa akakimbia na kuwa mkaaji mgeni katika nchi ya Midiani,+ ambako alizaa wana wawili.+

30 “Na miaka 40 ilipotimia, malaika akamtokea katika mwali wa moto wa mti wa miiba katika nyika ya Mlima Sinai.+ 31 Sasa Musa alipouona akastaajabia maono hayo.+ Lakini alipokuwa akikaribia ili kuchunguza, sauti ya Yehova ikaja, 32 ‘Mimi ni Mungu wa mababu zako, Mungu wa Abrahamu na wa Isaka na wa Yakobo.’+ Akitetemeka, Musa hakuthubutu kuchunguza zaidi. 33 Yehova akamwambia, ‘Vua viatu kutoka miguuni, kwa maana mahali ambapo umesimama ni udongo mtakatifu.+ 34 Kwa hakika nimeona jinsi watu wangu walio Misri+ wanavyotendewa vibaya, nami nimesikia kuugua+ kwao na nimeshuka ili kuwakomboa.+ Na sasa njoo, nitakutuma uende Misri.’+ 35 Musa huyo, ambaye hao walimkana, wakisema, ‘Ni nani aliyekuweka wewe kuwa mtawala na mwamuzi?’+ mtu huyo Mungu alimtuma+ aende akiwa mtawala na pia mkombozi kwa mkono wa malaika aliyemtokea katika mti wa miiba. 36 Mtu huyo aliwaongoza watoke+ baada ya kufanya mambo ya ajabu na ishara katika Misri+ na katika Bahari Nyekundu+ na katika nyika kwa miaka 40.+

37 “Huyo ndiye Musa aliyewaambia wana wa Israeli, ‘Mungu atawainulia kutoka kati ya ndugu zenu nabii kama mimi.’+ 38 Huyo ndiye+ aliyekuja kuwa katikati ya kutaniko+ katika nyika pamoja na malaika+ aliyesema naye juu ya Mlima Sinai na pamoja na mababu zetu, naye akapokea maneno matakatifu+ yaliyo hai ili awape ninyi. 39 Mababu zetu walikataa kumtii, bali wakamsukuma kando+ na katika mioyo yao wakageuka kurudi Misri,+ 40 wakimwambia Haruni, ‘Tufanyie miungu iende mbele yetu. Kwa maana huyo Musa, aliyetuongoza kutoka katika nchi ya Misri, hatujui lililompata.’+ 41 Kwa hiyo wakafanya ndama siku hizo+ wakailetea hiyo sanamu dhabihu na kuanza kujifurahisha katika kazi za mikono yao.+ 42 Kwa hiyo Mungu akageuka na kuwakabidhi+ watoe utumishi mtakatifu kwa jeshi la mbinguni, kama vile ambavyo imeandikwa katika kitabu cha manabii,+ ‘Je, mimi ndiye mliyetolea wanyama na dhabihu nyikani kwa miaka 40, Ee nyumba ya Israeli?+ 43 Bali mlichukua hema la Moloki+ na nyota+ ya mungu Refani, maumbo mliyoyafanya ili kuyaabudu. Kwa sababu hiyo nitawahamishia+ ninyi ng’ambo ya Babiloni.’

44 “Mababu zetu walikuwa na hema la ushahidi nyikani, kama vile alivyotoa maagizo alipokuwa akisema na Musa ili kulifanya kulingana na mfano aliokuwa ameuona.+ 45 Na mababu zetu waliolirithi waliliingiza pamoja na Yoshua+ ndani ya nchi iliyomilikiwa na mataifa,+ ambayo Mungu aliyafukuza kutoka mbele ya mababu zetu.+ Lilibaki humo mpaka siku za Daudi. 46 Alipata kibali+ machoni pa Mungu na kuomba pendeleo la kuandaa makao+ kwa ajili ya Mungu wa Yakobo. 47 Hata hivyo, Sulemani alimjengea nyumba.+ 48 Ingawa hivyo, Aliye Juu Zaidi hakai katika nyumba zilizofanywa kwa mikono;+ kama vile nabii anavyosema, 49 ‘Mbingu ni kiti changu cha ufalme,+ nayo dunia ni kiti cha miguu+ yangu. Mtanijengea nyumba ya aina gani? Asema Yehova. Au mahali pangu pa kupumzika pako wapi?+ 50 Mikono yangu ilifanya vitu vyote hivi, sivyo?’+

51 “Ninyi watu wenye shingo ngumu na wasiotahiriwa katika mioyo+ na masikio, sikuzote mnaipinga roho takatifu; kama mababu zenu walivyofanya, ndivyo ninyi mnavyofanya.+ 52 Ni yupi kati ya manabii ambaye mababu zenu hawakumtesa?+ Ndiyo, waliwaua+ wale waliotangaza kimbele kuhusu kuja kwa Aliye mwadilifu,+ ambaye ninyi sasa mmemsaliti na kumuua,+ 53 ninyi mliopokea Sheria kama ilivyopitishwa na malaika+ lakini hamkuishika.”

54 Basi, waliposikia mambo hayo wakahisi wamechomwa mioyoni+ mwao na kuanza kumsagia+ meno yao. 55 Lakini yeye, akiwa amejaa roho takatifu, akakaza macho mbinguni, akaona utukufu wa Mungu na wa Yesu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume+ wa Mungu, 56 naye akasema: “Tazameni! Ninaziona mbingu zimefunguka+ na Mwana wa binadamu+ akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume+ wa Mungu.” 57 Ndipo wakapaaza sauti ya juu na kuweka mikono yao juu ya masikio yao,+ wakamrukia wote pamoja. 58 Na baada ya kumtupa nje ya jiji,+ wakaanza kumtupia mawe.+ Na wale mashahidi+ wakaweka chini mavazi yao ya nje miguuni pa kijana aliyeitwa Sauli.+ 59 Nao wakaendelea kumtupia Stefano mawe huku akiomba na kusema: “Bwana Yesu, pokea roho yangu.”+ 60 Ndipo akapiga magoti yake, akapaaza sauti kubwa: “Yehova, usiwahesabie dhambi hii.”+ Na baada ya kusema hayo akalala usingizi katika kifo.

8 Naye Sauli alikuwa akikubaliana na kuuawa kwake.+

Katika siku hiyo mateso+ makubwa yakatokea juu ya kutaniko lililokuwa katika Yerusalemu; wote isipokuwa mitume walitawanywa+ kotekote katika maeneo ya Yudea na Samaria. 2 Lakini wanaume wenye kumheshimu Mungu wakamchukua Stefano kwenda kumzika,+ nao wakafanya maombolezo+ makubwa juu yake. 3 Ingawa hivyo, Sauli akaanza kushughulikia kutaniko kwa njia mbaya kabisa. Akawa akivamia nyumba moja baada ya nyingine, akiwakokota nje wanaume na wanawake, na kuwatia gerezani.+

4 Hata hivyo, wale waliokuwa wametawanywa wakapita katika nchi wakitangaza habari njema ya lile neno.+ 5 Filipo akashuka kwenda jiji la Samaria+ na kuanza kuwahubiria juu ya Kristo. 6 Kwa umoja umati ulikuwa ukisikiliza kwa makini mambo ambayo Filipo alikuwa akisema huku ukisikiliza na kutazama ishara alizokuwa akifanya. 7 Kwa maana wengi walikuwa na roho wachafu,+ na roho hao walikuwa wakipaaza sauti kubwa na kutoka. Zaidi ya hayo, wengi waliokuwa wamepooza+ na walio vilema waliponywa. 8 Kwa hiyo kukawa na shangwe kubwa katika jiji hilo.+

9 Sasa katika jiji hilo kulikuwa na mtu fulani aliyeitwa Simoni, ambaye, kabla ya hili, alikuwa akifanya ufundi wa uchawi+ na kushangaza taifa la Samaria, akisema yeye mwenyewe alikuwa mtu mkuu.+ 10 Na wote, mdogo kwa mkubwa, walikuwa wakimkazia uangalifu na kusema: “Mtu huyu ndiye Nguvu za Mungu, zinazoweza kuitwa Kuu.” 11 Kwa hiyo walikuwa wakimsikiliza kwa sababu alikuwa amewashangaza kwa muda fulani kwa ufundi wake wa uchawi. 12 Lakini walipomwamini Filipo, aliyekuwa akitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu+ na juu ya jina la Yesu Kristo, wakabatizwa, wanaume na pia wanawake.+ 13 Simoni mwenyewe pia akawa mwamini, na, baada ya kubatizwa, akawa akimhudumia Filipo+ daima; naye alishangaa kuona ishara na kazi kubwa zenye nguvu zikitendeka.

14 Wakati mitume katika Yerusalemu waliposikia kwamba Samaria ilikuwa imelikubali neno la Mungu,+ wakawatuma Petro na Yohana kwao; 15 na hawa wakashuka kwenda na kusali kwa ajili yao wapate roho takatifu.+ 16 Kwa maana ilikuwa bado haijamwangukia yeyote kati yao, bali walikuwa wamebatizwa tu katika jina la Bwana Yesu.+ 17 Ndipo wakaanza kuweka mikono yao juu yao,+ nao wakaanza kupokea roho takatifu.

18 Sasa Simoni alipoona kwamba roho ilitolewa kupitia kuwekewa mikono ya mitume, aliwatolea pesa,+ 19 akisema: “Nipeni mimi pia mamlaka hii, ili yeyote ambaye nitaweka mikono yangu juu yake apate kupokea roho takatifu.” 20 Lakini Petro akamwambia: “Fedha yako na iangamie pamoja nawe, kwa sababu ulitaka kupata zawadi ya bure ya Mungu kwa kutumia pesa.+ 21 Wewe huna sehemu wala fungu katika jambo hili, kwa maana moyo wako si mnyoofu machoni pa Mungu.+ 22 Kwa hiyo, tubu ubaya wako huu, na umwombe Yehova dua+ ili, ikiwezekana, upate kusamehewa hila ya moyo wako; 23 kwa maana ninaona wewe ni nyongo yenye sumu+ na kifungo cha ukosefu wa uadilifu.”+ 24 Simoni akajibu akasema: “Ninyi, mwombeni Yehova dua+ kwa ajili yangu ili hata moja kati ya mambo mliyosema lisinipate.”

25 Kwa hiyo, walipokuwa wametoa ushahidi kikamili na wakiwa wamelisema neno la Yehova, wakarudi Yerusalemu, nao wakaenda wakitangaza habari njema kwenye vijiji vingi vya Wasamaria.+

26 Hata hivyo, malaika+ wa Yehova akasema na Filipo, akamwambia: “Ondoka uende upande wa kusini kwenye barabara inayoshuka kutoka Yerusalemu mpaka Gaza.” (Hii ni barabara ya jangwani.) 27 Ndipo akaondoka akaenda, na, tazama! towashi+ Mwethiopia,+ mwanamume aliye na mamlaka chini ya Kandake malkia wa Waethiopia, na ambaye alikuwa juu ya hazina yote ya malkia. Huyo alikuwa ameenda Yerusalemu kuabudu,+ 28 lakini alikuwa anarudi naye alikuwa ameketi katika gari lake, akimsoma kwa sauti kubwa nabii Isaya.+ 29 Kwa hiyo roho ikamwambia+ Filipo: “Karibia ujiunge na gari hili.” 30 Filipo akakimbia kandokando na kumsikia akimsoma kwa sauti kubwa nabii Isaya, naye akasema: “Je, wewe kwa kweli unaelewa unayoyasoma?” 31 Akasema: “Kwa kweli, ninawezaje kuelewa, mtu fulani asiponiongoza?” Naye akamsihi Filipo apande na kuketi pamoja naye. 32 Sasa kifungu cha Andiko alichokuwa akisoma kwa sauti kubwa kilikuwa hiki: “Kama kondoo aliletwa machinjioni, na kama mwana-kondoo asiye na sauti mbele ya mwenye kumnyoa, ndivyo huyo asivyofungua kinywa chake.+ 33 Wakati wa kufedheheshwa kwake hukumu iliondolewa mbali naye.+ Ni nani atakayeeleza kirefu habari za kizazi chake? Kwa sababu uhai wake unaondolewa kutoka duniani.”+

34 Yule towashi akamjibu akamwambia Filipo: “Ninakuomba, Nabii anasema hivyo juu ya nani? Juu yake mwenyewe au juu ya mtu mwingine?” 35 Filipo akafungua kinywa chake,+ akaanza na Andiko+ hilo, akamtangazia habari njema juu ya Yesu. 36 Sasa walipokuwa wakienda juu ya ile barabara, wakafika mahali penye maji, na towashi akasema: “Tazama! Maji; ni nini kinachonizuia nisibatizwe?”+ 37 —— 38 Ndipo akaamuru gari lisimame, nao wote wawili wakashuka na kuingia ndani ya maji, Filipo na pia towashi; naye akambatiza. 39 Walipokuwa wamepanda kutoka ndani ya maji, roho ya Yehova ikamwondoa Filipo upesi,+ na towashi hakumwona tena kamwe, kwa maana aliendelea kwenda zake akishangilia. 40 Lakini Filipo akaonekana Ashdodi, naye akaenda akipita katika eneo hilo na kuendelea kuyatangazia+ majiji yote habari njema mpaka alipofika Kaisaria.+

9 Lakini Sauli, bado akiwatisha wanafunzi+ wa Bwana na akitaka kuwaua,+ akamwendea kuhani mkuu 2 na kumwomba barua za kwenda kwenye masinagogi katika Damasko, ili apate kuwaleta Yerusalemu wakiwa wamefungwa wowote ambao angewapata walio wa Ile Njia,+ wanaume na wanawake.

3 Basi alipokuwa akisafiri, akakaribia Damasko, na ghafula nuru kutoka mbinguni ikamulika kumzunguka,+ 4 naye akaanguka chini na kusikia sauti ikimwambia: “Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa?”+ 5 Akasema: “Wewe ni nani, Bwana?” Akasema: “Mimi ni Yesu, ambaye wewe unatesa.+ 6 Hata hivyo, simama+ uingie jijini, nawe utaambiwa jambo unalopaswa kufanya.” 7 Basi wanaume waliokuwa wakisafiri pamoja naye+ walikuwa wamesimama wakiwa hawana la kusema,+ wakisikia, kwa kweli, sauti,+ lakini bila kumwona mtu yeyote. 8 Lakini Sauli akainuka, na ingawa macho yake yalikuwa yamefunguka hakuwa akiona kitu.+ Kwa hiyo wakamwongoza kwa kumshika mkono na kumpeleka Damasko. 9 Na kwa siku tatu hakuona kitu chochote,+ naye hakula wala kunywa.

10 Katika Damasko kulikuwa na mwanafunzi fulani aliyeitwa Anania,+ naye Bwana akamwambia katika maono: “Anania!” Akasema: “Mimi hapa, Bwana.” 11 Bwana akamwambia: “Ondoka, uende kwenye barabara inayoitwa Nyoofu, na kwenye nyumba ya Yuda tafuta mtu anayeitwa jina Sauli, kutoka Tarso.+ Kwa maana, tazama! anasali, 12 na katika maono amemwona mwanamume anayeitwa Anania akiingia na kuweka mikono yake juu yake ili apate kuona tena.”+ 13 Lakini Anania akajibu: “Bwana, nimesikia kutoka kwa wengi juu ya mtu huyu, mambo mengi mabaya aliyowatendea watakatifu wako katika Yerusalemu. 14 Naye hapa ana mamlaka kutoka kwa wakuu wa makuhani kuwatia vifungoni wale wote wanaoliitia jina lako.”+ 15 Lakini Bwana akamwambia: “Ondoka uende, kwa sababu mtu huyu ni chombo kilichochaguliwa+ kwangu ili kupeleka jina langu kwa mataifa+ na vilevile kwa wafalme+ na wana wa Israeli. 16 Kwa maana nitamwonyesha wazi ni mambo mangapi ambayo atateseke kwa ajili ya jina langu.”+

17 Kwa hiyo Anania akaenda zake na kuingia katika ile nyumba, naye akaweka mikono yake juu yake na kusema: “Sauli, ndugu, yule Bwana, yule Yesu aliyekutokea katika barabara uliyoijia, amenituma, ili upate kuona tena na kujazwa roho takatifu.”+ 18 Na mara moja kitu kilichoonekana kama magamba kikaanguka kutoka kwenye macho yake, naye akapata kuona tena; naye akasimama na kubatizwa, 19 naye akala chakula na kupata nguvu.+

Kwa siku kadhaa akapata kuwa pamoja na wanafunzi katika Damasko,+ 20 naye akaanza mara moja kumhubiri Yesu+ katika masinagogi, kwamba Huyu ndiye Mwana wa Mungu. 21 Lakini wote waliomsikia wakashangaa nao wakawa wakisema: “Je, huyu si yule mtu aliyewaangamiza+ wale walio katika Yerusalemu wanaoliitia jina hilo, na aliyekuwa amekuja hapa kwa kusudi hilo hilo, ili apate kuwapeleka wakiwa wamefungwa kwa wakuu wa makuhani?”+ 22 Lakini Sauli akaendelea kupata nguvu hata zaidi naye alikuwa akiwafadhaisha Wayahudi waliokuwa wakikaa Damasko alipokuwa akithibitisha kupatana na akili kwamba huyu ndiye Kristo.+

23 Sasa mwishoni mwa siku nyingi, Wayahudi walikata shauri pamoja kumwangamiza.+ 24 Hata hivyo, hila yao juu yake ikajulikana kwa Sauli. Lakini walikuwa pia wakiyaangalia sana malango mchana na pia usiku ili kumwangamiza.+ 25 Kwa hiyo wanafunzi wake wakamchukua na kumshusha usiku kupitia shimo ukutani, wakamshusha katika kapu.+

26 Alipofika Yerusalemu+ akafanya jitihada za kujiunga na wanafunzi; lakini wote walikuwa wakimwogopa, kwa sababu hawakuamini alikuwa mwanafunzi. 27 Kwa hiyo Barnaba akaja kumsaidia+ na kumpeleka kwa mitume, naye akawaambia kirefu jinsi alivyokuwa amemwona Bwana+ katika barabara, na kwamba alikuwa amesema naye,+ na jinsi alivyokuwa amesema kwa ujasiri katika jina la Yesu, kule Damasko.+ 28 Naye akakaa pamoja nao, akitembea ndani na nje katika Yerusalemu, akisema kwa ujasiri katika jina la Bwana;+ 29 naye alikuwa akiongea na kubishana na Wayahudi wenye kusema Kigiriki. Lakini hao wakawa wakijaribu kumwangamiza.+ 30 Akina ndugu walipogundua hilo, wakamshusha mpaka Kaisaria na kumtuma aende zake Tarso.+

31 Ndipo, kwa kweli, kutaniko+ kotekote katika Yudea na Galilaya na Samaria likaingia katika kipindi cha amani, likijengwa; nalo lilipokuwa likitembea katika kumwogopa Yehova+ na katika faraja ya roho takatifu+ likaendelea kuongezeka.

32 Sasa Petro alipokuwa akienda kupitia sehemu zote akashuka pia kwa watakatifu waliokuwa wakikaa Lida.+ 33 Huko akapata mwanamume fulani aliyeitwa Ainea, ambaye alikuwa amelala juu ya kitanda chake kwa miaka minane, kwa kuwa alikuwa amepooza. 34 Naye Petro akamwambia:+ “Ainea, Yesu Kristo anakuponya wewe.+ Simama, utandike kitanda chako.” Naye akasimama mara moja. 35 Na wale wote waliokuwa wakikaa Lida na katika nchi tambarare ya Sharoni+ wakamwona, nao wakageuka kumwelekea Bwana.+

36 Lakini katika Yopa+ kulikuwako mwanafunzi fulani aliyeitwa Tabitha, jina ambalo, linapotafsiriwa, linamaanisha Dorkasi. Huyo alizidi katika matendo mema+ na zawadi za rehema alizokuwa akitoa. 37 Lakini ikawa kwamba katika siku hizo alishikwa na ugonjwa akafa. Kwa hiyo wakamwosha na kumlaza katika chumba cha juu. 38 Sasa kwa kuwa Lida palikuwa karibu na Yopa,+ wanafunzi waliposikia kwamba Petro alikuwa katika jiji hilo wakatuma wanaume wawili kwake wakamsihi: “Tafadhali usikawie kuja kwetu.” 39 Ndipo Petro akaondoka na kwenda pamoja nao. Naye alipofika, wakampeleka katika chumba cha juu; na wajane wote wakajitokeza kwake wakilia na kuonyesha mavazi mengi ya ndani na mavazi ya nje+ ambayo Dorkasi alikuwa akitengeneza alipokuwa pamoja nao.+ 40 Lakini Petro akamtoa kila mtu nje,+ akapiga magoti, akasali, akaugeukia ule mwili, akasema: “Tabitha, inuka!” Akafungua macho yake na, alipomwona Petro, akaketi wima.+ 41 Petro akampa mkono wake, akamwinua,+ naye akawaita watakatifu na wajane na akamweka mbele yao akiwa hai.+ 42 Jambo hilo likajulikana kotekote katika Yopa, na wengi wakamwamini Bwana.+ 43 Petro akabaki Yopa+ siku kadhaa pamoja na mtu fulani anayeitwa Simoni, mtengenezaji wa ngozi.+

10 Sasa katika Kaisaria kulikuwa na mwanamume fulani aliyeitwa jina Kornelio, ofisa-jeshi+ wa kikosi+ cha Italia, kama kilivyokuwa kikiitwa, 2 mtu mwenye kuheshimu+ na kumwogopa+ Mungu pamoja na watu wote wa nyumba yake, naye aliwapa watu+ zawadi nyingi za rehema na kuomba dua kwa Mungu sikuzote.+ 3 Karibu tu na saa tisa+ ya mchana akaona wazi katika maono+ malaika+ wa Mungu akiingia kwake na kumwambia: “Kornelio!” 4 Mtu huyo akamtazama na, akiogopa, akasema: “Ni nini, Bwana?” Akamwambia: “Sala+ na zawadi zako za rehema zimepanda kama ukumbusho mbele za Mungu.+ 5 Kwa hiyo sasa tuma watu Yopa ukamwite Simoni anayeitwa Petro. 6 Mtu huyu ni mgeni wa Simoni, mtengenezaji wa ngozi, aliye na nyumba kando ya bahari.”+ 7 Mara tu malaika aliyesema naye alipokuwa ameondoka, akawaita wawili kati ya watumishi wake wa nyumbani na askari-jeshi mwenye kumwogopa Mungu kutoka kati ya wale waliokuwa wakimhudumia daima,+ 8 naye akawasimulia kila kitu na kuwatuma kwenda Yopa.+

9 Siku iliyofuata walipokuwa wakiendelea na safari yao na wakikaribia jiji hilo, Petro akapanda juu ya paa+ ya nyumba karibu saa sita ili kusali.+ 10 Lakini akaona njaa sana naye akataka kula. Walipokuwa wakitayarisha, akapata njozi+ 11 naye akaona mbingu imefunguliwa+ na chombo cha namna fulani kikishuka kama shuka kubwa la kitani, kikishushwa juu ya dunia kwa ncha zake nne; 12 na ndani yake mlikuwa namna zote za viumbe wenye miguu minne na vitu vinavyotambaa vya dunia na ndege wa mbinguni.+ 13 Na sauti ikamjia: “Simama, Petro, chinja ule!”+ 14 Lakini Petro akasema: “Sivyo hata kidogo, Bwana, kwa sababu sijakula kamwe kitu chochote kilichotiwa unajisi na kisicho safi.”+ 15 Na sauti ikasema tena naye, mara ya pili: “Wewe acha kuviita najisi+ vitu ambavyo Mungu ametakasa.” 16 Jambo hilo likatokea mara ya tatu, na mara hiyo kile chombo kikachukuliwa juu mbinguni.+

17 Basi Petro alipokuwa amefadhaika sana ndani yake juu ya maana ya maono aliyokuwa ameona, tazama! wale watu waliotumwa na Kornelio walikuwa wameuliza kuhusu nyumba ya Simoni na walikuwa wamesimama hapo langoni.+ 18 Nao wakapaaza sauti na kuuliza kama Simoni anayeitwa Petro alikuwa mgeni humo. 19 Petro alipokuwa akiwaza akilini mwake kuhusu yale maono, roho+ ikasema: “Tazama! Wanaume watatu wanakutafuta. 20 Hata hivyo, simama, ushuke na kwenda pamoja nao, nawe usiwe na shaka hata kidogo, kwa sababu nimewatuma.”+ 21 Kwa hiyo Petro akashuka kutoka ghorofani mpaka kwa wanaume hao na kusema: “Tazameni! Mimi ndiye mnayetafuta. Kwa nini mko hapa?” 22 Wakasema: “Kornelio, ofisa-jeshi, mwanamume mwadilifu na mwenye kumwogopa Mungu+ na mwenye sifa njema+ katika taifa lote la Wayahudi, malaika mtakatifu alimpa maagizo ya Mungu kwamba atume watu ili uitwe uje nyumbani kwake apate kuyasikia mambo utakayosema.” 23 Kwa hiyo akawakaribisha na kuwapa makao.

Siku iliyofuata akaondoka na kwenda pamoja nao, na baadhi ya akina ndugu waliokuwa wametoka Yopa wakaenda pamoja naye. 24 Siku ya pili yake akaingia Kaisaria. Bila shaka, Kornelio alikuwa akiwatarajia naye alikuwa amewaita pamoja jamaa zake na rafiki zake wa karibu sana. 25 Petro alipokuwa akiingia, Kornelio akakutana naye, akaanguka chini miguuni pake na kumsujudia. 26 Lakini Petro akamwinua, akisema: “Simama; mimi pia ni mwanadamu.”+ 27 Naye alipokuwa akiongea naye akaingia na kuwakuta watu wengi wakiwa wamekusanyika, 28 naye akawaambia: “Ninyi mnajua jinsi ilivyo kinyume cha sheria kwa Myahudi kujiunga na mtu wa jamii nyingine au kumkaribia;+ na bado Mungu amenionyesha sipaswi kumwita mtu yeyote kuwa najisi au si safi.+ 29 Kwa sababu hiyo nikaja, kwa kweli bila kupinga, nilipoitwa nije. Kwa hiyo ninawauliza ninyi ni sababu gani mliyoniitia.”

30 Basi Kornelio akasema: “Siku nne zilizopita kutoka saa hii nilikuwa nikisali katika nyumba yangu saa tisa,+ wakati, tazama! mwanamume aliyekuwa amevaa vazi linalong’aa+ alisimama mbele yangu 31 na kusema, ‘Kornelio, sala yako imesikiwa na kukubaliwa, nazo zawadi zako za rehema zimekumbukwa mbele za Mungu.+ 32 Kwa hiyo, tuma watu waende Yopa na kumwita Simoni, anayeitwa Petro.+ Mtu huyu ni mgeni katika nyumba ya Simoni, mtengenezaji wa ngozi, kando ya bahari.’+ 33 Kwa hiyo mara moja nikatuma watu kwako, nawe ukafanya vema kuja hapa. Na kwa hiyo wakati huu sisi sote tupo mbele za Mungu kuyasikia mambo yote ambayo umeamriwa na Yehova kusema.”+

34 Ndipo Petro akafungua kinywa chake na kusema: “Kwa hakika ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi,+ 35 bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.+ 36 Alituma+ neno kwa wana wa Israeli kuwatangazia habari njema ya amani+ kupitia Yesu Kristo: Huyu ni Bwana wa wengine wote.+ 37 Ninyi mnaijua habari iliyoongewa kotekote katika Yudea yote, kuanzia Galilaya baada ya ubatizo aliohubiri Yohana,+ 38 yaani, Yesu aliyekuwa ametoka Nazareti, jinsi Mungu alivyomtia mafuta kwa roho takatifu+ na nguvu, naye akaenda akipita katika nchi akitenda mema na kuwaponya wote waliokandamizwa na Ibilisi;+ kwa sababu Mungu alikuwa pamoja naye.+ 39 Nasi ni mashahidi wa mambo yote aliyoyafanya katika nchi ya Wayahudi na pia katika Yerusalemu; lakini walimwangamiza pia kwa kumtundika mtini.+ 40 Mungu alimfufua Huyu katika siku ya tatu na kumfunua,+ 41 si kwa watu wote, bali kwa mashahidi waliowekwa kimbele na Mungu,+ kwetu sisi, tuliokula na kunywa pamoja naye+ baada ya kufufuliwa kwake kutoka kwa wafu. 42 Pia, alituagiza sisi tuwahubirie+ watu na kutoa ushahidi kamili kwamba Huyu ndiye aliyeagizwa na Mungu kuwa mwamuzi wa walio hai na wafu.+ 43 Kwake yeye manabii wote hutoa ushahidi,+ kwamba kila mtu anayemwamini hupata msamaha wa dhambi kupitia jina lake.”+

44 Petro alipokuwa bado akisema juu ya mambo haya roho takatifu ikawaangukia wote waliokuwa wakisikia lile neno.+ 45 Na waaminifu waliokuwa wamekuja pamoja na Petro ambao walikuwa kati ya wale waliotahiriwa wakashangaa, kwa sababu zawadi ya bure ya roho takatifu ilikuwa ikimiminwa pia juu ya watu wa mataifa.+ 46 Kwa maana waliwasikia wakisema katika lugha na wakimtukuza Mungu.+ Ndipo Petro akajibu: 47 “Je, mtu yeyote anaweza kuyakataza maji kwamba hawa wasibatizwe+ ambao wameipokea roho takatifu kama vile sisi tulivyoipokea?” 48 Ndipo akawaamuru wabatizwe katika jina la Yesu Kristo.+ Kisha wakamwomba akae pamoja nao siku kadhaa.

11 Sasa mitume na ndugu waliokuwa katika Yudea wakasikia kwamba watu wa mataifa+ walikuwa pia wamepokea neno la Mungu. 2 Kwa hiyo Petro alipopanda mpaka Yerusalemu, waliokuwa wakiunga mkono kutahiriwa+ wakaanza kushindana naye, 3 wakisema aliingia ndani ya nyumba ya watu ambao hawakuwa wametahiriwa naye alikula pamoja nao. 4 Ndipo Petro akawaeleza waziwazi, akisema:

5 “Mimi nilikuwa katika jiji la Yopa nikisali, na katika njozi nikaona maono, chombo cha namna fulani kikishuka kama shuka kubwa la kitani, kikishushwa kwa ncha zake nne kutoka mbinguni, nacho kikaja moja kwa moja mahali nilipokuwa. 6 Nilipotazama ndani yake, nilichunguza na kuona viumbe vya dunia vyenye miguu minne na wanyama-mwitu na vitu vinavyotambaa na ndege wa mbinguni.+ 7 Pia nikasikia sauti ikiniambia, ‘Simama, Petro, chinja ule!’+ 8 Lakini nikasema, ‘Sivyo hata kidogo, Bwana, kwa sababu kitu najisi au kisicho safi hakijapata kamwe kuingia ndani ya kinywa changu.’+ 9 Mara ya pili sauti kutoka mbinguni ikajibu, ‘Wewe acha kuviita najisi vitu ambavyo Mungu ametakasa.’+ 10 Hilo likatokea mara ya tatu, na kila kitu kikavutwa juu tena kuingia mbinguni.+ 11 Pia, tazama! wakati huohuo wanaume watatu walikuwa wamesimama karibu na nyumba tuliyokuwamo, wakiwa wametumwa kutoka Kaisaria kuja kwangu.+ 12 Kwa hiyo roho+ ikaniambia niende pamoja nao, bila kuwa na shaka hata kidogo. Lakini ndugu sita hawa pia walikwenda pamoja nami, nasi tukaingia ndani ya nyumba ya mwanamume huyo.+

13 “Alitueleza jinsi alivyomwona malaika amesimama katika nyumba yake na kusema, ‘Tuma watu waende Yopa wakamwite Simoni anayeitwa Petro,+ 14 naye atasema nawe mambo ambayo yatakuwezesha wewe na watu wote wa nyumba yako kuokolewa.’+ 15 Lakini nilipoanza kusema, roho takatifu ikawaangukia kama vile ilivyoanguka pia juu yetu mwanzoni.+ 16 Ndipo nikayakumbuka maneno ya Bwana, jinsi alivyokuwa akisema, ‘Yohana alibatiza kwa maji,+ lakini ninyi mtabatizwa kwa roho takatifu.’+ 17 Kwa hiyo, ikiwa Mungu aliwapa hao zawadi ileile ya bure kama vile alivyotupa sisi pia ambao tumemwamini Bwana Yesu Kristo,+ mimi ni nani hata niweze kumzuia Mungu?”+

18 Basi waliposikia mambo hayo, wakakubali kimyakimya,+ nao wakamtukuza Mungu,+ wakisema: “Kwa hiyo, basi, Mungu ameruhusu toba kwa kusudi la uzima kwa watu wa mataifa pia.”+

19 Kwa sababu hiyo wale waliokuwa wametawanywa+ na dhiki iliyotokea kwa sababu ya Stefano wakapita kwenda mpaka Foinike+ na Kipro+ na Antiokia, lakini hawakusema lile neno kwa yeyote ila kwa Wayahudi tu.+ 20 Hata hivyo, kati yao kulikuwa na wanaume fulani wa Kipro na Kirene waliokuja Antiokia na kuanza kuongea na watu wenye kusema Kigiriki,+ wakitangaza habari njema ya Bwana Yesu.+ 21 Zaidi ya hayo, mkono wa Yehova+ ulikuwa pamoja nao, na hesabu kubwa ya waliopata kuwa waamini wakageuka kumwelekea Bwana.+

22 Kutaniko lililokuwa katika Yerusalemu likasikia juu yao, nao wakamtuma Barnaba+ mpaka Antiokia. 23 Alipofika na kuziona fadhili zisizostahiliwa+ za Mungu, akashangilia+ na kuanza kuwatia wote moyo waendelee katika Bwana wakiwa na azimio la moyoni;+ 24 kwa maana alikuwa mwanamume mwema na mwenye kujaa roho takatifu na imani. Na umati mkubwa ukaongezwa kwa Bwana.+ 25 Kwa hiyo akaenda zake mpaka Tarso+ ili kumtafuta Sauli+ 26 na, baada ya kumpata, akamleta Antiokia. Hivyo ikatukia kwamba kwa mwaka mzima wakakusanyika pamoja nao katika kutaniko na kufundisha umati mkubwa, na kule Antiokia ndipo ambapo kwa mara ya kwanza wanafunzi kwa uongozi wa kimungu waliitwa Wakristo.+

27 Basi katika siku hizo manabii+ walishuka kutoka Yerusalemu mpaka Antiokia. 28 Mmoja kati yao anayeitwa jina Agabo+ akasimama na kuonyesha kupitia roho kwamba njaa kali ilikuwa karibu kuja juu ya dunia nzima inayokaliwa;+ ambayo, kama ilivyo, ilitukia wakati wa Klaudio. 29 Kwa hiyo wanafunzi wakaamua, kila mmoja kwa kadiri ambayo yeyote angeweza kutoa,+ wafanye huduma ya kupeleka misaada+ kwa akina ndugu waliokuwa wakikaa Yudea; 30 nao wakafanya hivyo, wakaipeleka kwa wanaume wazee kwa mkono wa Barnaba na Sauli.+

12 Karibu na wakati huo Mfalme Herode alitumia mikono yake kuwatendea vibaya+ baadhi ya wale wa kutaniko. 2 Alimuua kwa upanga+ Yakobo ndugu ya Yohana.+ 3 Alipoona kuwa jambo hilo limewapendeza Wayahudi,+ akamkamata Petro pia. (Ikawa kwamba hizo zilikuwa siku za keki zisizo na chachu.)+ 4 Na alipomkamata, akamweka gerezani,+ akamkabidhi kwenye zamu nne za askari-jeshi wanne kila moja ili kumlinda, kwa kuwa alikusudia kumleta mbele ya watu baada ya pasaka.+ 5 Kwa hiyo Petro alikuwa gerezani; lakini kutaniko lilikuwa likisali+ kwa Mungu kwa juhudi nyingi kwa ajili yake.

6 Sasa Herode alipokuwa karibu kumtoa, usiku huo Petro alikuwa amelala akiwa amefungwa kwa minyororo miwili katikati ya askari-jeshi wawili, na walinzi mbele ya mlango walikuwa wakililinda gereza. 7 Lakini, tazama! malaika wa Yehova akasimama+ kando, na nuru ikang’aa katika chumba cha gereza. Akampiga Petro ubavuni, akamwamsha,+ akisema: “Amka upesi!” Na minyororo yake ikaanguka+ kutoka kwenye mikono yake. 8 Malaika+ akamwambia: “Jifunge kiuno na uvae viatu vyako.” Akafanya hivyo. Mwishowe akamwambia: “Vaa vazi+ lako la nje uendelee kunifuata.” 9 Naye akatoka na kuendelea kumfuata, lakini hakujua kwamba lililokuwa likitukia kupitia malaika lilikuwa halisi. Kwa kweli, alidhani alikuwa akiona maono.+ 10 Wakampita askari-mlinzi wa kwanza na wa pili wakafika kwenye lango la chuma linaloelekea jijini, nalo likafunguka lenyewe mbele yao.+ Na baada ya kutoka wakapita katika barabara moja, na mara malaika akamwacha. 11 Na Petro akarudiwa na fahamu, akasema: “Sasa ninajua hakika kwamba Yehova alimtuma+ malaika wake na kunikomboa+ kutoka mkononi mwa Herode na kutoka katika yote ambayo Wayahudi wote walikuwa wakitarajia.”

12 Na baada ya kufikiria jambo hilo, akaenda kwenye nyumba ya Maria mama ya Yohana aliyeitwa Marko,+ ambamo watu wengi walikuwa wamekusanyika na wakisali. 13 Alipopiga hodi kwenye mlango wa njia ya lango, kijakazi anayeitwa Roda akaja kujibu, 14 na, alipoitambua sauti ya Petro, hakulifungua lango kwa sababu ya shangwe, bali akakimbia ndani na kueleza kwamba Petro alikuwa amesimama mbele ya njia ya lango. 15 Wakamwambia: “Una wazimu.” Lakini akasisitiza kwa nguvu ndivyo ilivyokuwa. Wakaanza kusema: “Ni malaika wake.”+ 16 Lakini Petro akakaa hapo akibisha mlango. Walipofungua, wakamwona nao wakashangaa. 17 Lakini akawapungia+ mkono wanyamaze na kuwaambia kirefu jinsi Yehova alivyomtoa gerezani, naye akasema: “Waambieni Yakobo+ na akina ndugu mambo haya.” Ndipo akatoka, akasafiri kwenda mahali pengine.

18 Basi, mchana ulipofika,+ kulikuwa na msukosuko usio mdogo kati ya askari-jeshi kuhusu ni jambo gani kwa kweli lililokuwa limempata Petro. 19 Herode+ akamtafuta kwa bidii na, alipokosa kumpata, akawahoji walinzi na kuwaamuru wapelekwe kuadhibiwa;+ naye akashuka kwenda Yudea mpaka Kaisaria na kukaa huko kwa muda fulani.

20 Sasa yeye alitaka kupigana na watu wa Tiro na wa Sidoni. Kwa hiyo wakamjia kwa umoja na, baada ya kumshawishi Blasto, aliyekuwa msimamizi wa chumba cha kulala cha mfalme, wakaanza kutoa ombi la kutaka amani, kwa sababu nchi yao iligawiwa chakula+ kutoka katika kile cha mfalme. 21 Lakini siku fulani iliyowekwa Herode akajivika vazi la kifalme na kuketi juu ya kiti cha hukumu na kuanza kuwatolea hotuba ya watu wote. 22 Nao watu waliokusanyika wakaanza kupaaza sauti: “Ni sauti ya mungu, wala si ya mwanadamu!”+ 23 Papo hapo malaika wa Yehova akampiga,+ kwa sababu hakumpa Mungu utukufu;+ naye akaliwa na wadudu akakata pumzi.

24 Lakini neno+ la Yehova likaendelea kukua na kuenea.+

25 Naye Barnaba+ na Sauli, baada ya kutimiza kikamili ile huduma ya misaada+ katika Yerusalemu, wakarudi na kumchukua pamoja nao Yohana,+ aliyeitwa Marko.

13 Basi katika Antiokia kulikuwa na manabii+ na walimu katika kutaniko la mahali hapo, Barnaba na vilevile Simioni aliyeitwa Nigeri, na Lukio+ wa Kirene, na Manaeni aliyeelimishwa pamoja na Herode mtawala wa wilaya, na Sauli. 2 Walipokuwa wakimhudumia+ Yehova hadharani na kufunga, roho takatifu ikasema: “Kati ya watu wote wekeni kando Barnaba na Sauli+ kwa ajili yangu kwa kazi ambayo nimewaitia wao.” 3 Ndipo wakafunga na kusali na kuweka mikono+ yao juu yao, wakawaacha waende zao.

4 Basi watu hawa, waliotumwa na roho takatifu, wakashuka kwenda Seleukia, na kutoka huko wakasafiri kwa mashua kwenda Kipro. 5 Na walipofika Salami wakaanza kulitangaza neno la Mungu katika masinagogi ya Wayahudi. Pia walikuwa na Yohana+ akiwatumikia.

6 Walipokuwa wamepita katika kisiwa chote mpaka Pafo, wakakutana na mwanamume fulani, mlozi, nabii wa uwongo,+ Myahudi ambaye jina lake lilikuwa Bar-Yesu, 7 naye alikuwa pamoja na liwali Sergio Paulo, mwanamume mwenye akili. Akawaita Barnaba na Sauli, naye mtu huyu akataka kulisikia neno la Mungu. 8 Lakini Elima mlozi (hivyo, kwa kweli, ndivyo jina lake linavyotafsiriwa) akaanza kuwapinga,+ akitafuta kumgeuzia mbali yule liwali kutoka kwenye ile imani. 9 Sauli, ambaye pia ni Paulo, akiwa amejaa roho takatifu, akamtazama 10 na kusema: “Ewe mtu mwenye kujaa kila namna ya upunjaji na kila namna ya ulaghai, wewe mwana wa Ibilisi, wewe adui wa kila jambo la uadilifu, je, hutaacha kuzipotoa njia zilizo sawa za Yehova?+ 11 Hivyo, basi, tazama! mkono wa Yehova uko juu yako wewe, nawe utakuwa kipofu, usiweze kuiona nuru ya jua kwa kipindi fulani.” Mara moja ukungu mzito na giza vikamwangukia, naye akazunguka akitafuta watu wa kumwongoza wakiwa wamemshika mkono.+ 12 Ndipo yule liwali,+ alipoona jambo lililokuwa limetukia, akawa mwamini, kwa kuwa alistaajabishwa na fundisho la Yehova.

13 Hao watu, pamoja na Paulo, sasa wakasafiri baharini kutoka Pafo na kufika Perga katika Pamfilia.+ Lakini Yohana+ akawaacha na kurudi+ Yerusalemu. 14 Hata hivyo, wao wakaendelea kutoka Perga na kuja Antiokia katika Pisidia nao wakaingia ndani ya sinagogi+ siku ya sabato, wakaketi. 15 Baada ya kusoma Sheria+ na Manabii mbele ya watu wote maofisa-wasimamizi+ wa sinagogi wakawatuma watu kwao, wakisema: “Wanaume, akina ndugu, ikiwa kuna neno lolote la kitia moyo mlilo nalo kwa ajili ya watu, lisemeni.” 16 Kwa hiyo Paulo akasimama, akapunga+ mkono wake, akasema:

“Wanaume, Waisraeli na ninyi wengine ambao mnamwogopa Mungu, sikieni.+ 17 Mungu wa watu hawa Israeli aliwachagua mababu zetu, naye akawainua watu hao walipokuwa wakikaa katika nchi ya kigeni katika nchi ya Misri na kuwatoa katika hiyo kwa mkono ulioinuliwa.+ 18 Na kwa kipindi cha karibu miaka 40+ akavumilia jinsi walivyotenda nyikani. 19 Baada ya kuyaangamiza mataifa saba katika nchi ya Kanaani, aligawanya nchi yao kwa kura:+ 20 yote haya wakati wa karibu miaka 450.

“Na baada ya mambo hayo aliwapa waamuzi mpaka nabii Samweli.+ 21 Lakini tangu hapo na kuendelea wakadai mfalme,+ na Mungu akawapa Sauli mwana wa Kishi, mwanamume wa kabila la Benyamini,+ kwa miaka 40. 22 Na baada ya kumwondoa huyo,+ akawainulia Daudi kuwa mfalme,+ ambaye alitoa ushahidi kumhusu na kusema, ‘Nimemwona Daudi mwana wa Yese,+ mtu anayekubalika kwa moyo wangu,+ atakayefanya mambo yote ambayo ninatamani.’+ 23 Kutoka katika uzao+ wa mwanamume huyu kulingana na ahadi yake Mungu ameletea Israeli mwokozi,+ Yesu, 24 baada ya Yohana,+ kabla ya kuingia kwake Huyo,+ akiwa amekwisha kuhubiri hadharani kwa watu wote wa Israeli ubatizo unaoonyesha toba. 25 Lakini Yohana alipokuwa akitimiza mwendo wake, akawa akisema ‘Mnadhani mimi ni nani? Mimi si yeye. Lakini, tazameni! mmoja anakuja baada yangu ambaye viatu vya miguu yake mimi sistahili kuvifungua.’+

26 “Wanaume, akina ndugu, ninyi wana wa ukoo wa Abrahamu na wale wengine kati yenu ambao mnamwogopa Mungu, neno la wokovu huu limeletwa kwetu sisi.+ 27 Kwa maana wakaaji wa Yerusalemu na watawala wao hawakumjua Huyu,+ bali, walipokuwa wakitenda wakiwa waamuzi, walitimiza mambo yaliyosemwa na Manabii,+ mambo ambayo husomwa kwa sauti kubwa kila Sabato, 28 na, ijapokuwa hawakupata sababu yoyote ya kumuua+ walidai kwa Pilato kwamba auawe.+ 29 Basi, walipokuwa wametimiza mambo yote yaliyoandikwa juu yake,+ walimshusha chini kutoka kwenye mti+ na kumlaza katika kaburi.+ 30 Lakini Mungu akamfufua kutoka kwa wafu;+ 31 na kwa siku nyingi akaonekana kwa wale ambao walikuwa wamepanda kwenda pamoja naye kutoka Galilaya mpaka Yerusalemu, ambao sasa ni mashahidi wake kwa watu.+

32 “Na kwa hiyo sisi tunawatangazia ninyi habari njema juu ya ahadi iliyotolewa kwa mababu,+ 33 kwamba Mungu ameitimiza kabisa kwetu sisi tulio watoto wao kwa kuwa alimfufua Yesu;+ hata kama vile ambavyo imeandikwa katika zaburi ya pili, ‘Wewe ni mwanangu, mimi nimekuwa Baba yako leo.’+ 34 Na jambo hilo la kwamba yeye alimfufua kutoka kwa wafu akikusudiwa asirudi tena kwenye uharibifu, yeye amelisema katika njia hii, ‘Nitawapa ninyi fadhili zenye upendo kwa Daudi ambazo ni za uaminifu.’+ 35 Kwa sababu hiyo anasema pia katika zaburi nyingine, ‘Hutamruhusu mshikamanifu wako aone uharibifu.’+ 36 Kwa maana Daudi,+ kwa upande mmoja, alitumikia mapenzi kamili ya Mungu katika kizazi chake mwenyewe na kulala katika kifo na alilazwa pamoja na mababu zake na kuona uharibifu.+ 37 Kwa upande mwingine, yule ambaye Mungu alimfufua hakuona uharibifu.+

38 “Kwa hiyo acheni ijulikane kwenu, akina ndugu, kwamba kupitia Huyo msamaha wa dhambi unatangazwa kwenu;+ 39 na kwamba kutokana na mambo yote ambayo ninyi hamngeweza kutangazwa kuwa bila hatia kwa njia ya sheria ya Musa,+ kila mtu anayeamini anatangazwa kuwa bila hatia kwa njia ya Huyu.+ 40 Kwa hiyo hakikisheni kwamba yale yaliyosemwa katika Manabii hayaji juu yenu, 41 ‘Oneni, ninyi wenye kudharau, mstaajabie, na mtoweke, kwa sababu ninafanya tendo katika siku zenu, tendo ambalo hamtaliamini hata kidogo hata yeyote akiwaeleza kirefu.’ ”+

42 Basi walipokuwa wakitoka, watu wakaanza kusihi waambiwe mambo hayo siku ya sabato inayofuata.+ 43 Kusanyiko la sinagogi lilipomalizika, wengi kati ya Wayahudi na kati ya wageuzwa-imani waliomwabudu Mungu wakawafuata Paulo na Barnaba,+ ambao walisema nao na kuanza kuwahimiza+ waendelee kubaki katika fadhili zisizostahiliwa za Mungu.+

44 Siku ya Sabato iliyofuata karibu jiji lote lilikusanyika pamoja kulisikia neno la Yehova.+ 45 Wayahudi walipoona umati, walijawa na wivu+ na kuanza kuyapinga kwa kukufuru mambo yaliyokuwa yakisemwa na Paulo.+ 46 Na kwa hiyo, wakiongea kwa ujasiri, Paulo na Barnaba wakasema: “Ilikuwa lazima neno la Mungu lihubiriwe kwenu kwanza.+ Kwa kuwa mnalisukumia mbali+ kutoka kwenu na hamjioni kuwa mnastahili uzima wa milele, tazameni! tunawageukia mataifa.+ 47 Kwa kweli, Yehova ameweka amri juu yetu kwa maneno haya, ‘Nimewaweka ninyi kuwa nuru ya mataifa,+ ili muwe wokovu mpaka sehemu ya mwisho ya dunia.’ ”+

48 Wale wa mataifa waliposikia jambo hilo, wakaanza kushangilia na kulitukuza neno la Yehova,+ na wale wote waliokuwa na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele wakawa waamini.+ 49 Zaidi ya hayo, neno la Yehova likaendelea kupelekwa kotekote katika nchi yote.+ 50 Lakini Wayahudi+ wakawachochea wanawake wenye kusifika waliomwabudu Mungu na wakuu wa jiji, nao wakazusha mateso+ juu ya Paulo na Barnaba na kuwatupa nje ya mipaka yao. 51 Hawa wakawakung’utia mavumbi kutoka miguuni pao+ na kwenda Ikoniamu. 52 Na wanafunzi wakaendelea kujawa na shangwe+ na roho takatifu.

14 Basi katika Ikoniamu+ wakaingia pamoja katika sinagogi+ la Wayahudi na kusema kwa namna ambayo iliufanya umati mkubwa wa Wayahudi na pia Wagiriki+ kuwa waamini. 2 Lakini Wayahudi ambao hawakuamini wakachochea+ na kuwa na uvutano mbaya juu ya nafsi za watu wa mataifa dhidi ya akina ndugu.+ 3 Kwa hiyo wakatumia muda mrefu wakisema kwa ujasiri kwa mamlaka ya Yehova, aliyetoa ushahidi kuhusu neno la fadhili zake zisizostahiliwa kwa kuruhusu ishara na mambo ya ajabu kutukia kupitia kwa mikono yao.+ 4 Hata hivyo, umati wa jiji ukagawanyika, na baadhi yao walikuwa upande wa Wayahudi lakini wengine upande wa mitume. 5 Basi watu wa mataifa na pia Wayahudi pamoja na watawala wao walipojaribu kwa jeuri kuwatendea kwa dharau na kuwatupia mawe,+ 6 wao, walipojulishwa jambo hilo, wakakimbilia+ majiji ya Likaonia, Listra na Derbe na nchi yenye kuzunguka; 7 na huko wakaendelea kutangaza habari njema.+

8 Sasa katika Listra mwanamume fulani aliyekuwa amelemaa miguu alikuwa ameketi, kilema tangu alipokuwa katika tumbo la uzazi la mama yake,+ naye alikuwa hajatembea kamwe. 9 Mtu huyo alikuwa akimsikiliza Paulo akisema, ambaye, alipomtazama na kuona kwamba ana imani+ ya kuponywa, 10 akasema kwa sauti kubwa: “Simama wima kwa miguu yako.” Naye akaruka na kuanza kutembea.+ 11 Na umati, walipoona jambo ambalo Paulo alikuwa amefanya, wakapaaza sauti, wakisema katika lugha ya Kilikaonia: “Miungu+ imekuwa kama binadamu nayo imeshuka kwetu!” 12 Naye Barnaba wakamwita Zeu, lakini Paulo wakamwita Herme, kwa kuwa ndiye aliyekuwa akiongoza katika kusema. 13 Na kuhani wa Zeu, ambaye hekalu lake lilikuwa mbele ya jiji, akaleta ng’ombe-dume na shada za maua kwenye malango naye alikuwa anataka kutoa dhabihu+ pamoja na umati.

14 Hata hivyo, mitume Barnaba na Paulo waliposikia jambo hilo, wakayararua mavazi yao ya nje na kuruka ndani ya umati, wakipaaza sauti 15 na kusema: “Wanaume, kwa nini mnafanya mambo haya? Sisi pia ni wanadamu+ tulio na udhaifu+ uleule kama ninyi, nasi tunawatangazia ninyi habari njema, ili mgeuke kutoka kwa mambo haya ya bure+ mpate kumjia Mungu aliye hai,+ aliyefanya mbingu+ na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo. 16 Katika vizazi vilivyopita yeye aliwaruhusu mataifa yote waendelee kutembea katika njia zao,+ 17 ijapokuwa, kwa kweli, hakujiacha mwenyewe bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema,+ akiwapa ninyi mvua+ kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo yenu kikamili kwa chakula na uchangamfu.”+ 18 Na bado kwa kusema mambo haya wakauzuia umati kwa shida, wasiwatolee dhabihu.

19 Lakini Wayahudi wakafika kutoka Antiokia na Ikoniamu wakaushawishi umati,+ nao wakampiga Paulo kwa mawe na kumkokota nje ya jiji, wakiwazia alikuwa amekufa.+ 20 Hata hivyo, wanafunzi walipomzunguka, akasimama na kuingia ndani ya jiji. Na siku iliyofuata akaondoka pamoja na Barnaba kwenda Derbe.+ 21 Na baada ya kulitangazia jiji hilo habari njema na kufanya wanafunzi+ wengi, wakarudi Listra na Ikoniamu na Antiokia, 22 wakizitia nguvu nafsi za wanafunzi,+ wakiwatia moyo kubaki katika imani na kusema: “Lazima tuingie katika ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.”+ 23 Zaidi ya hayo, wakawaweka rasmi wanaume wazee+ kwa ajili yao katika kila kutaniko, wakatoa sala pamoja na kufunga,+ na kuwakabidhi kwa Yehova+ ambaye walikuwa wamemwamini.

24 Nao wakapita katika Pisidia na kuingia Pamfilia,+ 25 na, baada ya kulisema neno katika Perga, wakashuka kwenda Atalia. 26 Na kutoka huko wakasafiri kwenda Antiokia,+ walikokuwa wamekabidhiwa kwenye fadhili zisizostahiliwa za Mungu kwa ajili ya kazi waliyokuwa wameifanya kikamili.+

27 Walipokuwa wamefika na wakiwa wamelikusanya kutaniko pamoja, wakaeleza mambo mengi+ ambayo Mungu alikuwa amefanya kupitia kwao, na kwamba alikuwa amewafungulia mataifa mlango wa kuingia katika imani.+ 28 Kwa hiyo wakatumia muda usio mdogo wakiwa pamoja na wanafunzi.

15 Na watu fulani wakashuka kutoka Yudea+ na kuanza kuwafundisha ndugu: “Msipotahiriwa+ kulingana na desturi ya Musa,+ hamwezi kuokolewa.” 2 Lakini kulipokuwa kumetokea mtengano usio mdogo na bishano kati ya Paulo na Barnaba pamoja nao, wakapanga Paulo na Barnaba na wengine kati yao wapande kwenda kwa mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu+ kuhusu bishano hilo.

3 Basi, baada ya kusindikizwa na kutaniko,+ watu hao wakaenda zao wakipitia Foinike na pia Samaria, wakieleza kirefu kugeuka kwa watu wa mataifa,+ nao walikuwa wakitokeza shangwe kubwa kwa akina ndugu wote.+ 4 Walipofika Yerusalemu walikaribishwa kwa fadhili+ na kutaniko na mitume na wanaume wazee, nao wakaeleza mambo mengi ambayo Mungu alikuwa ameyafanya kupitia kwao.+ 5 Lakini, baadhi ya wale wa madhehebu ya Mafarisayo waliokuwa wameamini wakasimama kutoka kwenye viti vyao na kusema: “Ni lazima kuwatahiri+ na kuwaamuru washike sheria ya Musa.”+

6 Na mitume na wanaume wazee wakakusanyika pamoja ili waliangalie jambo hilo.+ 7 Basi bishano+ kubwa lilipokuwa limetukia, Petro akasimama na kuwaambia: “Wanaume, akina ndugu, ninyi mnajua vema kwamba tangu siku za zamani Mungu alichagua kati yenu kwamba kupitia kinywa changu watu wa mataifa wasikie neno la habari njema na kuamini;+ 8 na Mungu, anayeujua moyo,+ alitoa ushahidi kwa kuwapa wao roho takatifu,+ kama vile alivyotupa sisi pia. 9 Naye hakufanya tofauti hata kidogo kati yetu na wao,+ bali aliisafisha mioyo yao kwa imani.+ 10 Kwa hiyo, sasa kwa nini mnamjaribu Mungu kwa kuweka juu ya shingo za wanafunzi nira+ ambayo mababu zetu wala sisi hatukuweza kubeba?+ 11 Kinyume chake, sisi tunaamini kwamba tutaokolewa kupitia fadhili zisizostahiliwa+ za Bwana Yesu katika njia ileile kama watu hao pia.”+

12 Ndipo umati mzima ukanyamaza, nao wakaanza kuwasikiliza Barnaba na Paulo wakieleza ishara nyingi na mambo mengi ya ajabu ambayo Mungu alifanya kupitia kwao katikati ya mataifa.+ 13 Walipomaliza kusema, Yakobo akajibu, akisema: “Wanaume, akina ndugu, nisikieni.+ 14 Simioni+ ameeleza kikamili jinsi Mungu kwa mara ya kwanza alivyoelekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake.+ 15 Na maneno ya Manabii yanakubaliana na jambo hili, kama vile ambavyo imeandikwa, 16 ‘Baada ya mambo hayo nitarudi na kukijenga upya kibanda cha Daudi ambacho kimeanguka chini; nami nitayajenga upya mabomoko yake na kukisimamisha tena,+ 17 ili watu wanaobaki wamtafute Yehova kwa bidii, pamoja na watu wa mataifa yote, watu wanaoitwa kwa jina langu, asema Yehova, anayefanya mambo haya,+ 18 yanayojulikana tangu zamani za kale.’+ 19 Kwa hiyo nimeamua kutowataabisha wale wa kutoka katika mataifa wanaomgeukia Mungu,+ 20 bali kuwaandikia wajiepushe na vitu vilivyochafuliwa na sanamu,+ na uasherati,+ na kile kilichonyongwa,+ na damu.+ 21 Kwa maana tangu nyakati za kale katika jiji baada ya jiji Musa amekuwa na wale wanaomhubiri, kwa sababu yeye husomwa kwa sauti kubwa katika masinagogi kila siku ya sabato.”+

22 Ndipo mitume na wanaume wazee pamoja na kutaniko lote wakapendelea kutuma wanaume waliochaguliwa kutoka kati yao mpaka Antiokia pamoja na Paulo na Barnaba, yaani, Yuda aliyeitwa Barsaba+ na Sila, wanaume wenye kuongoza kati ya akina ndugu; 23 na kwa mkono wao wakaandika:

“Mitume na wanaume wazee, akina ndugu, kwa wale ndugu katika Antiokia+ na Siria na Kilikia+ ambao ni wa kutoka kwa mataifa: Salamu! 24 Kwa kuwa tumesikia kwamba baadhi ya wale waliotoka kati yetu wamewataabisha ninyi kwa maneno mengi,+ wakijaribu kupindua nafsi zenu, ijapokuwa sisi hatukuwapa maagizo yoyote,+ 25 sisi tumefikia kauli moja+ nasi tumependelea kuchagua wanaume tuwatume kwenu pamoja na wapendwa wetu, Barnaba na Paulo,+ 26 watu ambao wametoa nafsi zao kwa ajili ya jina la Bwana wetu Yesu Kristo.+ 27 Kwa hiyo tunawatuma Yuda na Sila,+ ili wao pia wapate kueleza mambo hayohayo kwa maneno.+ 28 Kwa maana roho takatifu+ na sisi wenyewe tumependelea tusiwaongezee ninyi mzigo+ zaidi, ila mambo haya ya lazima, 29 kuendelea kujiepusha na vitu vilivyotolewa dhabihu kwa sanamu+ na damu+ na vitu vilivyonyongwa+ na uasherati.+ Mkijiepusha kwa uangalifu na mambo haya,+ mtafanikiwa. Afya njema kwenu!”

30 Basi, watu hawa walipoachwa waende, wakashuka kwenda Antiokia, nao wakaukusanya umati pamoja na kuwapa barua hiyo.+ 31 Baada ya kuisoma, walishangilia juu ya kitia-moyo hicho.+ 32 Nao Yuda na Sila, kwa kuwa wao wenyewe walikuwa manabii+ pia, wakawatia moyo akina ndugu kwa hotuba nyingi na kuwatia nguvu.+ 33 Kwa hiyo, baada ya kukaa huko kwa muda fulani, ndugu hao wakawaacha waende kwa amani+ kwa wale waliokuwa wamewatuma. 34 —— 35 Hata hivyo, Paulo na Barnaba wakaendelea kukaa Antiokia+ wakifundisha na kutangaza habari njema ya neno la Yehova, wakiwa pamoja na wengine wengi pia.+

36 Sasa baada ya siku kadhaa Paulo akamwambia Barnaba: “Zaidi ya mambo yote, na turudi tuwatembelee akina ndugu katika kila moja la majiji ambamo tulitangaza neno la Yehova tuone jinsi walivyo.”+ 37 Barnaba alikuwa ameazimia kumchukua Yohana pia, aliyeitwa Marko.+ 38 Lakini Paulo hakuona kwamba inafaa kumchukua huyo pamoja nao, kwa kuwa alikuwa amewaacha kule Pamfilia+ na hakuwa ameenda pamoja nao kwenye kazi. 39 Ndipo kukatokea hasira kali, hivi kwamba wakatengana; Barnaba+ akamchukua Marko pamoja naye na kusafiri kwenda Kipro.+ 40 Paulo akamchagua Sila+ akaondoka kwenda zake baada ya kuwa amekabidhiwa na akina ndugu kwenye fadhili zisizostahiliwa za Yehova.+ 41 Lakini akapitia Siria na Kilikia, akiyatia nguvu makutaniko.+

16 Kwa hiyo akafika Derbe na pia Listra.+ Na, tazama! mwanafunzi fulani aliyeitwa Timotheo+ alikuwa huko, mwana wa mwanamke Myahudi aliye mwamini lakini wa baba Mgiriki, 2 naye alishuhudiwa vema na akina ndugu katika Listra na Ikoniamu. 3 Paulo alitamani mtu huyu aende pamoja naye, naye akamchukua na kumtahiri+ kwa sababu ya Wayahudi waliokuwa katika sehemu hizo, kwa maana wote walijua kwamba baba yake ni Mgiriki. 4 Basi walipoendelea kusafiri kupitia katika majiji walikuwa wakiwapa wale waliokuwa huko maagizo yaliyokuwa yameamuliwa na mitume na wanaume wazee waliokuwa katika Yerusalemu ili wayashike.+ 5 Kwa hiyo, kwa kweli, makutaniko yakaendelea kufanywa imara katika imani+ na kuongezeka hesabu siku baada ya siku.

6 Zaidi ya hayo, wakapitia Frigia na nchi ya Galatia,+ kwa sababu walikatazwa na roho takatifu wasiseme lile neno katika wilaya ya Asia. 7 Tena, walipofika Misia wakafanya jitihada za kuingia Bithinia,+ lakini roho ya Yesu haikuwaruhusu. 8 Kwa hiyo wakapita Misia na kushuka mpaka Troa.+ 9 Na usiku maono+ yakamtokea Paulo: mwanamume fulani Mmakedonia alikuwa amesimama akimsihi na kusema: “Vuka uingie Makedonia utusaidie.” 10 Basi mara tu alipokuwa amekwisha kuona maono hayo, tukajaribu kuingia Makedonia,+ tukikata kauli kwamba Mungu alikuwa ametuita tuwatangazie habari njema.

11 Kwa hiyo tukasafiri baharini kutoka Troa na kuja kwa safari ya moja kwa moja mpaka Samothrake, lakini siku iliyofuata tukaja mpaka Neapoli, 12 na kutoka huko mpaka Filipi,+ koloni, ambalo ni jiji kuu la wilaya ya Makedonia.+ Tukakaa katika jiji hili kwa siku kadhaa. 13 Na siku ya sabato tukatoka nje ya lango kando ya mto, ambapo tulikuwa tukifikiri kwamba palikuwa na mahali pa sala; nasi tukaketi na kuanza kusema na wanawake waliokuwa wamekusanyika. 14 Na mwanamke fulani anayeitwa Lidia, muuzaji wa nguo za rangi ya zambarau, wa jiji la Thiatira+ aliyekuwa mwabudu wa Mungu, alikuwa akisikiliza, na Yehova akafungua wazi moyo+ wake asikilize kwa makini mambo yaliyokuwa yakisemwa na Paulo. 15 Basi yeye na watu wa nyumbani mwake walipobatizwa,+ akasema hivi kwa kusihi: “Ikiwa ninyi mmeniona kuwa mwaminifu kwa Yehova, ingieni ndani ya nyumba yangu mkae.”+ Naye akatushurutisha kwelikweli.+

16 Na ikatukia kwamba tulipokuwa tukienda pale mahali pa sala, kijakazi fulani mwenye roho,+ roho mwovu wa uaguzi,+ akakutana nasi. Yeye alikuwa akiwapatia mabwana zake faida+ nyingi kwa kufanya ufundi wa kubashiri. 17 Kijakazi huyo alikuwa akimfuata Paulo na sisi akipaaza sauti+ kwa maneno haya: “Watu hawa ni watumwa wa Mungu Aliye Juu Zaidi, wanaowatangazia ninyi njia ya wokovu.” 18 Akaendelea kufanya hivyo kwa siku nyingi. Mwishowe Paulo akachoshwa,+ akageuka na kumwambia huyo roho: “Ninakuagiza katika jina la Yesu Kristo umtoke.”+ Naye akatoka saa hiyohiyo.+

19 Basi, mabwana zake walipoona kwamba tumaini lao la kupata faida lilikuwa limeondoka,+ wakamshika Paulo na Sila wakawakokota na kuwapeleka sokoni kwa watawala,+ 20 wakawapeleka mpaka kwa mahakimu wa raia, wakasema: “Watu hawa wanasumbua+ sana jiji letu, wao wakiwa ni Wayahudi, 21 nao wanatangaza desturi+ ambazo si halali kwetu kuzikubali au kuzitenda, kwa kuwa sisi ni Waroma.” 22 Nao umati ukasimama pamoja dhidi yao; na wale mahakimu wa raia, baada ya kuyararua mavazi yao ya nje, wakatoa amri wapigwe kwa fimbo.+ 23 Baada ya kuwapiga mapigo mengi,+ wakawatupa gerezani, wakimwagiza mlinzi wa jela awalinde.+ 24 Kwa sababu alipata agizo la namna hiyo, akawatupa ndani ya gereza+ la ndani zaidi na kuifunga miguu yao katika mikatale.+

25 Lakini karibu na katikati ya usiku+ Paulo na Sila walikuwa wakisali na kumsifu Mungu kwa wimbo;+ ndiyo, wafungwa walikuwa wakiwasikia. 26 Kwa ghafula tetemeko kubwa la nchi likatukia, hivi kwamba misingi ya jela ikatikiswa. Zaidi ya hayo, milango yote ikafunguka mara moja, na vifungo vya wote vikafunguka.+ 27 Mlinzi wa jela, alipoamka kutoka usingizini na kuona milango ya gereza ilikuwa imefunguka, akauchomoa upanga wake na alikuwa karibu kujiua,+ akiwazia kwamba wafungwa walikuwa wametoroka.+ 28 Lakini Paulo akapaaza sauti kubwa, akisema: “Usijiumize,+ kwa maana sisi sote tupo hapa!” 29 Kwa hiyo akaomba taa akaruka ndani na, akitetemeka, akaanguka chini+ mbele ya Paulo na Sila. 30 Naye akawaleta nje na kusema: “Mabwana zangu, nifanye+ nini ili niokolewe?” 31 Wakasema: “Mwamini Bwana Yesu nawe utaokolewa,+ wewe na watu wa nyumba yako.”+ 32 Nao wakamwambia neno la Yehova pamoja na wale wote walio katika nyumba yake.+ 33 Naye akawachukua pamoja naye katika saa hiyo ya usiku akaosha mapigo yao; na, wote, yeye na walio wake wakabatizwa+ bila kukawia. 34 Naye akawaleta ndani ya nyumba yake na kutandika meza mbele yao, naye akashangilia sana pamoja na watu wote wa nyumba yake kwa kuwa sasa alikuwa amemwamini Mungu.

35 Ilipokuwa mchana mahakimu wa raia+ wakawatuma maofisa wa polisi wakaseme: “Wafungue wale watu.” 36 Kwa hiyo mlinzi wa jela akamweleza Paulo maneno yao: “Mahakimu wa raia wamewatuma watu kwamba ninyi wawili mfunguliwe. Kwa hiyo, sasa, tokeni mwende zenu kwa amani.” 37 Lakini Paulo akawaambia: “Walitupiga viboko hadharani bila kuhukumiwa kuwa wenye hatia, sisi tulio Waroma,+ na kututupa gerezani; na je, sasa wanatufukuza kwa siri? Hapana, hata kidogo! lakini acha wao wenyewe waje watutoe nje.” 38 Kwa hiyo wale maofisa wa polisi wakawaeleza mahakimu wa raia maneno hayo. Nao wakaogopa waliposikia kwamba watu hao walikuwa Waroma.+ 39 Kwa hiyo wakaja na kuwasihi na, baada ya kuwatoa nje, wakawaomba waondoke katika jiji hilo. 40 Lakini wakatoka katika gereza hilo na kwenda nyumbani kwa Lidia, nao walipowaona akina ndugu wakawatia moyo,+ wakaondoka.

17 Sasa wakasafiri kupitia Amfipoli na Apolonia wakaja mpaka Thesalonike,+ ambako kulikuwa na sinagogi la Wayahudi. 2 Basi kulingana na desturi ya Paulo+ akaingia ndani walimokuwa, na kwa sabato tatu akajadiliana nao kwa kutumia Maandiko,+ 3 akieleza na kuthibitisha kwa marejeo kwamba ilikuwa lazima Kristo ateseke+ na kufufuliwa kutoka kwa wafu,+ akisema: “Huyu ndiye Kristo,+ Yesu huyu ninayewatangazia ninyi.” 4 Ikawa kwamba baadhi yao wakawa waamini+ na kujiunga na Paulo na Sila,+ na umati mkubwa kati ya Wagiriki waliomwabudu Mungu na si wachache kati ya wanawake wenye vyeo waliofanya hivyo.

5 Lakini Wayahudi wakawa na wivu,+ wakashirikiana na wanaume fulani waovu kati ya wazururaji wa sokoni na kufanyiza kikundi chenye ghasia ili kuzusha fujo jijini.+ Nao wakaishambulia nyumba ya Yasoni+ na kuanza kujaribu kuwaleta mbele ya watu wenye kufanya ghasia. 6 Walipowakosa wakamkokota Yasoni na akina ndugu fulani na kuwapeleka kwa watawala wa jiji, wakipaaza sauti hivi: “Watu hawa ambao wameipindua+ dunia inayokaliwa wapo hapa pia, 7 na Yasoni amewakaribisha. Na watu wote hawa wanapingana na maagizo+ ya Kaisari, wakisema kuna mfalme+ mwingine, Yesu.” 8 Kwa kweli walifadhaisha huo umati na watawala wa jiji waliposikia mambo haya; 9 na kwanza baada ya kuchukua dhamana ya kutosha kutoka kwa Yasoni na wale wengine wakawaacha waende zao.

10 Mara moja wakati wa usiku+ akina ndugu wakatuma Paulo na Sila pia mpaka Beroya, na hawa, walipofika, wakaingia katika sinagogi la Wayahudi. 11 Sasa watu hawa walikuwa wasikivu kuliko wale wa Thesalonike, kwa maana walilipokea neno kwa hamu kubwa zaidi ya akili, wakiyachunguza+ Maandiko+ kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo.+ 12 Kwa hiyo wengi kati yao wakawa waamini, na pia walioamini kati ya wanawake Wagiriki wenye kusifika+ na kati ya wanaume si wachache. 13 Lakini Wayahudi kutoka Thesalonike walipopata habari kwamba Paulo alitangaza neno la Mungu katika Beroya pia, wakaja huko pia ili kuchochea+ na kuwafadhaisha+ watu. 14 Ndipo akina ndugu wakamsindikiza Paulo mara moja mpaka baharini;+ lakini Sila na Timotheo pia wakabaki nyuma huko. 15 Hata hivyo, wale waliokuwa wakimsindikiza Paulo wakamleta mpaka Athene na, baada ya kupokea amri kwamba Sila na Timotheo+ wamfuate upesi iwezekanavyo, wakaondoka.

16 Basi Paulo alipokuwa akiwangojea katika Athene, roho yake ikaudhika+ ndani yake alipoona kwamba jiji hilo lilikuwa limejaa sanamu. 17 Kwa hiyo akaanza kujadiliana katika sinagogi pamoja na Wayahudi+ na watu wengine waliomwabudu Mungu na kila siku sokoni+ pamoja na wale waliokuwapo. 18 Lakini watu fulani kati ya Waepikurea na wanafalsafa+ Wastoa pia wakawa wanaongea naye kwa mabishano, na baadhi yao walikuwa wakisema: “Mpiga-domo huyu angependa kueleza jambo gani?”+ Wengine: “Anaonekana kuwa mtangazaji wa miungu migeni.” Kwa sababu alikuwa akitangaza habari njema ya Yesu na ufufuo.+ 19 Kwa hiyo wakamshika na kumpeleka Areopago, wakisema: “Je, tunaweza kujua ni fundisho gani hili jipya+ unalosema? 20 Kwa maana unaanzisha mambo yaliyo mageni masikioni mwetu. Kwa hiyo tunataka kujua mambo haya yanamaanisha nini.”+ 21 Kwa kweli, Waathene wote na wageni waliokuwa wakikaa huko kwa muda hawakuwa wakitumia wakati wao wa starehe wakifanya chochote ila kuambiana jambo au kusikiliza jambo jipya. 22 Basi Paulo akasimama katikati ya Areopago+ na kusema:

“Wanaume wa Athene, ninaona kwamba katika mambo yote mnaonekana kuwa wenye mwelekeo zaidi wa kuogopa miungu+ kuliko wengine. 23 Kwa mfano, nilipokuwa nikipita njiani na kutazama kwa uangalifu vitu vyenu vya ibada, niliona pia madhabahu ambayo ilikuwa imeandikwa ‘Kwa Mungu Asiyejulikana.’ Kwa hiyo kile mnachokipa ujitoaji-kimungu bila kujua, hicho ninawatangazia ninyi. 24 Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, akiwa, kama Huyu alivyo, Bwana wa mbingu na dunia,+ hakai katika mahekalu yaliyofanywa kwa mikono,+ 25 wala hatumikiwi kwa mikono ya binadamu kana kwamba anahitaji kitu chochote,+ kwa sababu yeye mwenyewe huwapa watu wote uhai+ na pumzi+ na vitu vyote. 26 Naye alifanya kutoka kwa mtu mmoja+ kila taifa+ la watu, ili wakae juu ya uso wa dunia nzima,+ naye aliamuru nyakati+ na mipaka ya makao ya watu,+ 27 ili wao wamtafute Mungu,+ ikiwa wangeweza kupapasa-papasa wakimtafuta na kwa kweli wampate,+ ijapokuwa, kweli, hayuko mbali sana na kila mmoja wetu. 28 Kwa maana kupitia kwake tuna uhai na tunaenda na kuwako,+ hata kama vile ambavyo watu fulani ambao ni washairi+ kati yenu wamesema, ‘Kwa maana sisi pia ni uzao wake.’

29 “Kwa hiyo, kwa kuwa sisi ni uzao wa Mungu,+ hatupaswi kuwazia kwamba Mungu+ ni kama dhahabu au fedha au jiwe, kama kitu kilichochongwa kwa ufundi na mtungo wa mwanadamu.+ 30 Ni kweli, Mungu ameachilia mbali nyakati hizo za kutojua,+ lakini sasa anawaambia wanadamu wote kila mahali kwamba wanapaswa kutubu.+ 31 Kwa sababu ameweka siku ambayo katika hiyo anakusudia kuihukumu+ kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia kwa mwanamume ambaye amemweka rasmi, naye ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua+ kutoka kwa wafu.”

32 Basi, waliposikia juu ya ufufuo wa wafu, wengine kati yao wakaanza kudhihaki,+ huku wengine wakisema: “Tutakusikiliza tena juu ya jambo hili wakati mwingine.” 33 Hivyo Paulo akatoka katikati yao, 34 lakini wanaume fulani wakajiunga naye na kuwa waamini, kati yao pia wakiwa ni Dionisio, mwamuzi wa mahakama ya Areopago,+ na mwanamke mmoja aliyeitwa Damari, na wengine mbali na hao.

18 Baada ya hayo akaondoka Athene na kuja Korintho. 2 Naye akamkuta Myahudi fulani anayeitwa Akila,+ mzaliwa wa Ponto ambaye alikuwa amekuja hivi karibuni kutoka Italia,+ na Prisila mke wake, kwa sababu Klaudio+ alikuwa ameagiza Wayahudi wote waondoke Roma. Kwa hiyo akawaendea 3 na kwa sababu ya kuwa wa kazi ileile akakaa nyumbani kwao, nao wakafanya kazi,+ kwa maana kazi yao ilikuwa ya kutengeneza mahema. 4 Hata hivyo, yeye alikuwa akitoa hotuba katika sinagogi+ kila sabato na alikuwa akiwashawishi Wayahudi na Wagiriki.

5 Basi, Sila+ na Timotheo+ pia waliposhuka kutoka Makedonia, Paulo akaanza kushughulika sana na lile neno, akiwatolea Wayahudi ushahidi ili kuthibitisha kwamba Yesu ndiye Kristo.+ 6 Lakini walipoendelea kupinga na kutukana,+ akayakung’uta mavazi+ yake na kuwaambia: “Damu+ yenu na iwe juu ya vichwa vyenu wenyewe. Mimi ni safi.+ Tangu sasa na kuendelea nitaenda kwa watu wa mataifa.”+ 7 Basi akahama huko na kuingia katika nyumba ya mwanamume anayeitwa Titio Yusto, mwabudu wa Mungu, ambaye nyumba yake ilikuwa inashikana na sinagogi. 8 Lakini Krispo+ ofisa-msimamizi wa sinagogi akawa mwamini katika Bwana, na ndivyo na watu wote wa nyumba yake. Na wengi kati ya Wakorintho waliosikia wakaanza kuamini na kubatizwa. 9 Zaidi ya hayo, wakati wa usiku Bwana akamwambia Paulo+ kupitia maono: “Usiogope, bali endelea kusema wala usinyamaze, 10 kwa sababu mimi nipo pamoja na wewe+ na hakuna mtu atakayekushambulia ili kukutendea jambo baya; kwa maana nina watu wengi katika jiji hili.” 11 Kwa hiyo akakaa huko bila kuondoka kwa mwaka mmoja na miezi sita, akifundisha kati yao neno la Mungu.

12 Sasa Galio alipokuwa liwali+ wa Akaya, Wayahudi wakasimama kwa umoja dhidi ya Paulo na kumwongoza kwenye kiti cha hukumu,+ 13 wakisema: “Mtu huyu huongoza watu kinyume cha sheria+ kwenye sadikisho lingine katika kumwabudu Mungu.” 14 Lakini Paulo alipokuwa akitaka kufungua kinywa chake, Galio akawaambia Wayahudi: “Kama kwa kweli lingekuwa ni kosa fulani au tendo baya la uhalifu, enyi Wayahudi, ningekuwa na sababu ya kuwavumilia ninyi. 15 Lakini kama ni mabishano juu ya maneno na majina+ na sheria+ kati yenu, amueni ninyi wenyewe. Mimi sitaki kuwa mwamuzi wa mambo haya.” 16 Ndipo akawafukuza kutoka mbele ya kiti cha hukumu. 17 Kwa hiyo wote wakamshika Sosthene+ ofisa-msimamizi wa sinagogi na kuanza kumpiga mbele ya kiti cha hukumu. Lakini Galio hakujihangaisha hata kidogo na mambo hayo.

18 Hata hivyo, baada ya kukaa siku kadhaa zaidi, Paulo aliwaaga akina ndugu naye akaendelea kusafiri kwenda Siria, na pamoja naye Prisila na Akila, kwa kuwa nywele za kichwa chake zilikuwa zimekatwa+ katika Kenkrea,+ kwa maana alikuwa ameweka nadhiri. 19 Kwa hiyo wakafika Efeso, naye akawaacha huko; lakini yeye mwenyewe akaingia ndani ya sinagogi+ akajadiliana na Wayahudi. 20 Ijapokuwa waliendelea kumwomba akae kwa muda mrefu zaidi, hakukubali 21 bali akawaaga+ na kuwaambia: “Nitarudi kwenu tena, ikiwa Yehova anapenda.”+ Naye akasafiri baharini kutoka Efeso 22 na kushuka mpaka Kaisaria. Naye akapanda kwenda, akalisalimu kutaniko, na kushuka kwenda Antiokia.

23 Na alipokuwa amekaa huko kwa wakati fulani akaondoka na kwenda kutoka mahali mpaka mahali kupitia nchi ya Galatia+ na Frigia,+ akiwatia nguvu+ wanafunzi wote.

24 Sasa Myahudi fulani anayeitwa Apolo,+ mzaliwa wa Aleksandria, mwanamume mfasaha, akafika Efeso; naye alikuwa mwenye ujuzi mwingi sana wa Maandiko.+ 25 Mwanamume huyu alikuwa amefundishwa njia ya Yehova kwa mdomo, kwa kuwa alikuwa amewaka roho,+ akaanza kusema na kuyafundisha kwa usahihi mambo juu ya Yesu, lakini akiwa anaufahamu ubatizo+ wa Yohana tu. 26 Na mwanamume huyo akaanza kusema kwa ujasiri katika sinagogi. Prisila na Akila+ walipomsikia, wakamchukua na kumfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu. 27 Tena, kwa sababu alikuwa akitaka kuvuka aingie Akaya, akina ndugu wakawaandikia wanafunzi, wakiwahimiza wamkaribishe kwa fadhili. Kwa hiyo alipofika huko, akawasaidia+ sana wale waliokuwa wameamini kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa+ za Mungu; 28 kwa maana kwa juhudi nyingi alithibitisha kikamili hadharani kuwa Wayahudi ni wenye makosa, huku akionyesha kwa Maandiko+ kwamba Yesu alikuwa ndiye Kristo.+

19 Ikawa, Apolo+ alipokuwa Korintho, Paulo akapita barani na kushuka mpaka Efeso,+ akakuta wanafunzi fulani; 2 akawaambia: “Je, mlipokea roho takatifu+ mlipokuwa waamini?” Wakamwambia: “Lo! hatujapata kusikia kamwe kama kuna roho takatifu.”+ 3 Naye akasema: “Basi, mlibatizwa katika nini?” Wakasema: “Katika ubatizo wa Yohana.”+ 4 Paulo akasema: “Yohana alibatiza kwa ubatizo unaoonyesha toba,+ akiwaambia watu wamwamini yule ambaye angekuja baada yake,+ yaani, Yesu.” 5 Waliposikia hilo, wakabatizwa katika jina la Bwana Yesu.+ 6 Na Paulo alipoweka mikono+ yake juu yao, roho takatifu ikaja juu yao, nao wakaanza kusema katika lugha na kutoa unabii.+ 7 Wote pamoja walikuwa wanaume karibu kumi na wawili.

8 Akaingia katika sinagogi,+ akasema kwa ujasiri kwa miezi mitatu, akitoa hotuba na kutumia ushawishi kuhusu ufalme+ wa Mungu. 9 Lakini wengine walipoendelea kujifanya wenyewe wagumu na kutoamini,+ wakisema vibaya juu ya Ile Njia+ mbele ya umati, akaondoka kwao+ na kuwatenga wanafunzi kutoka kwao,+ kila siku akitoa hotuba nyingi katika jumba la shule ya Tirano. 10 Jambo hilo lilitukia kwa muda wa miaka miwili,+ hivi kwamba wale wote waliokuwa wakikaa katika wilaya ya Asia+ wakasikia neno la Bwana, Wayahudi na Wagiriki pia.

11 Na Mungu akazidi kufanya kazi za nguvu zinazozidi za kawaida kupitia mikono ya Paulo,+ 12 hivi kwamba hata nguo na vitambaa vilichukuliwa kutoka katika mwili wake na kupelekwa kwa watu wenye kuugua,+ na magonjwa yakawaacha, na roho waovu wakatoka.+ 13 Lakini watu fulani kati ya Wayahudi wenye kuzunguka-zunguka waliozoea kazi ya kufukuza roho waovu+ pia wakachukua daraka la kuliitia jina la Bwana Yesu+ juu ya wale wenye roho waovu, wakisema: “Mimi ninawaagiza+ ninyi kwa uzito kwa Yesu ambaye Paulo humhubiri.” 14 Sasa kulikuwa na wana saba wa Skewa, mkuu wa makuhani wa Kiyahudi, wakifanya jambo hilo. 15 Lakini roho mwovu akawajibu, akawaambia: “Mimi ninamjua Yesu+ nami ninamfahamu Paulo;+ lakini ninyi ni nani?” 16 Ndipo mtu huyo ambaye huyo roho mwovu alikuwa ndani yake akawarukia,+ akawazidi nguvu mmoja baada ya mwingine, na kuwashinda, hivi kwamba wakakimbia kutoka nyumba hiyo wakiwa uchi na wakiwa wameumizwa. 17 Jambo hilo likajulikana na wote, Wayahudi na Wagiriki pia waliokaa katika Efeso; na woga+ ukawaingia hao wote, na jina la Bwana Yesu likaendelea kutukuzwa.+ 18 Na wengi kati ya wale waliokuwa waamini wakawa wanakuja na kuungama+ na kueleza juu ya mazoea yao waziwazi. 19 Kwa kweli, hesabu kubwa ya wale waliozoea kufanya ufundi wa uchawi+ wakaleta pamoja vitabu vyao wakaviteketeza mbele ya kila mtu. Nao wakapiga pamoja hesabu za bei zake na kupata vikiwa na thamani ya vipande 50,000 vya fedha. 20 Hivyo katika njia yenye nguvu neno la Yehova likazidi kukua na kusitawi.+

21 Sasa mambo hayo yalipokuwa yametimizwa, Paulo akakusudia katika roho yake kwamba, baada ya kupitia Makedonia+ na Akaya, angefunga safari kwenda Yerusalemu,+ akisema: “Baada ya kufika huko lazima pia nione Roma.”+ 22 Kwa hiyo akawatuma wawili kati ya wale waliomhudumia, Timotheo+ na Erasto,+ waende Makedonia lakini yeye mwenyewe akakawia kwa wakati fulani katika wilaya ya Asia.

23 Wakati huo kukatokea mvurugo+ usio mdogo kuhusu Ile Njia.+ 24 Kwa maana mtu fulani anayeitwa jina Demetrio, fundi wa fedha, kwa kufanya vihekalu vya fedha vya Artemi aliwapa mafundi mapato ya faida+ isiyo ndogo; 25 naye akawakusanya hao na wale waliofanya kazi ya kutengeneza vitu vya namna hiyo+ na kusema: “Wanaume, ninyi mnajua vema kwamba sisi tumepata mafanikio yetu kutokana na biashara hii.+ 26 Pia, mnaona na kusikia jinsi si katika Efeso+ tu, bali pia katika karibu wilaya yote ya Asia, Paulo huyu ameshawishi umati mkubwa na kuwageuza kwenye kauli nyingine, akisema kwamba wale waliofanywa kwa mikono+ si miungu. 27 Zaidi ya hayo, kuna hatari si kwamba tu kazi hii yetu itapata sifa mbaya bali pia hekalu la Artemi,+ mungu mkuu wa kike, litaonwa kuwa si kitu na hata utukufu wake ambao wilaya yote ya Asia na dunia inayokaliwa huuabudu utashushwa uwe si kitu hivi karibuni.” 28 Waliposikia jambo hilo na kujawa na hasira, watu hao wakaanza kupaaza sauti, wakisema: “Artemi wa Waefeso ni mkuu!”

29 Kwa hiyo jiji likajaa mvurugo, na kwa umoja wakatimua mbio na kuingia jumba la maonyesho, wakawachukua kwa nguvu pamoja nao Gayo na Aristarko,+ Wamakedonia, wasafiri waliokuwa wakiandamana na Paulo. 30 Naye Paulo alitaka kuingia walimokuwa watu, lakini wanafunzi hawakumruhusu. 31 Hata baadhi ya wakuu wa sherehe na michezo, waliokuwa wakimwonyesha urafiki, wakatuma watu kwake na kuanza kumwomba asijihatarishe katika mahali pa michezo. 32 Kwa kweli, wengine walikuwa wakipaaza sauti wakisema jambo moja na wengine wakisema lingine;+ kwa maana kusanyiko lilikuwa katika mvurugo, na walio wengi kati yao hawakujua kwa nini walikuwa wamekusanyika. 33 Kwa hiyo wakiwa pamoja wakamtoa Aleksanda katikati ya umati, Wayahudi wakimsukuma mbele kwa nguvu; na Aleksanda akapunga mkono naye alikuwa akitaka kujitetea mbele ya watu. 34 Lakini walipotambua kwamba alikuwa Myahudi, wote wakapaaza sauti moja kwa karibu saa mbili wakisema: “Artemi wa Waefeso ni mkuu!”+

35 Mwishowe, karani wa jiji alipokuwa ameunyamazisha+ umati, akasema: “Watu wa Efeso, kwa kweli ni nani kati ya wanadamu ambaye hajui kwamba jiji la Efeso ndilo mtunza-hekalu wa Artemi mkuu na wa sanamu iliyoanguka kutoka mbinguni? 36 Kwa hiyo, kwa kuwa mambo haya hayawezi kukanushwa, inafaa mtulie na msitende haraka.+ 37 Kwa maana mmewaleta watu hawa ambao hawaibi katika mahekalu wala hawamkufuru mungu wetu wa kike. 38 Kwa hiyo ikiwa Demetrio+ na mafundi walio pamoja naye wana kesi juu ya mtu fulani, siku za mahakama+ hufanywa na kuna maliwali;+ acheni walete mashtaka mtu juu ya mwenzake. 39 Lakini, ikiwa mnatafuta jambo lolote zaidi ya hilo, lazima liamuliwe katika kusanyiko la kawaida. 40 Kwa maana kwa kweli tunakabili hatari ya kushtakiwa uchochezi wa uasi kuhusu tukio la leo, kukiwa hakuna msingi wowote mmoja tulio nao utakaoturuhusu tutoe sababu ya kikundi hiki chenye machafuko.” 41 Na alipokuwa amesema mambo hayo,+ akaliagiza kusanyiko liende.+

20 Sasa baada ya ghasia hizo kutulia, Paulo akatuma watu wawaite wanafunzi, na alipokuwa amewatia moyo na kuwaaga,+ akasafiri na kuingia Makedonia.+ 2 Baada ya kupitia sehemu hizo na kuwatia moyo wale walio huko kwa maneno mengi,+ akaingia Ugiriki. 3 Na alipokuwa amekaa huko kwa miezi mitatu, kwa sababu hila+ ilikuwa imetungwa juu yake na Wayahudi alipokuwa karibu kusafiri kwenda Siria, akaamua kurudi kupitia Makedonia. 4 Hawa waliandamana naye, Sopatro+ mwana wa Piro wa Beroya, Aristarko+ na Sekundo wa Wathesalonike, na Gayo wa Derbe, na Timotheo,+ na kutoka wilaya ya Asia Tikiko+ na Trofimo.+ 5 Hao wakatangulia, wakatungojea huko Troa;+ 6 lakini sisi tukaanza kusafiri baharini kutoka Filipi baada ya siku za keki zisizo na chachu,+ nasi tukawafikia huko Troa+ katika muda wa siku tano; na huko tukakaa siku saba.

7 Siku ya kwanza+ ya juma, tulipokuwa tumekusanyika pamoja ili kupata mlo, Paulo akaanza kuwahutubia, kwa kuwa alipaswa kuondoka siku inayofuata; naye akarefusha hotuba yake mpaka katikati ya usiku. 8 Kwa hiyo kulikuwa na taa nyingi katika chumba cha juu+ tulipokuwa tumekusanyika pamoja. 9 Kijana fulani anayeitwa Eutiko, aliyekuwa ameketi dirishani, akalala usingizi mzito huku Paulo akiendelea kuongea, naye akalemewa na usingizi, akaanguka chini kutoka ghorofa ya tatu akaokotwa akiwa amekufa. 10 Lakini Paulo akashuka kutoka ghorofani, akajitupa juu yake+ akamkumbatia na kusema: “Acheni kufanya kelele, kwa maana nafsi yake imo ndani yake.”+ 11 Akapanda ghorofani, akapata mlo na kula chakula, na baada ya kuongea kwa muda mrefu, mpaka mapambazuko, mwishowe akaondoka. 12 Basi wakamchukua huyo mvulana akiwa hai wakafarijiwa kupita kiasi.

13 Sasa tukaenda kwenye mashua na kusafiri mpaka Aso, ambako tulikusudia kumpandisha Paulo chomboni, kwa maana, baada ya kutoa maagizo hayo, yeye mwenyewe alikusudia kwenda kwa miguu. 14 Kwa hiyo alipotufikia katika Aso, tukampandisha chomboni na kwenda mpaka Mitilene; 15 tukasafiri kutoka huko siku iliyofuata, tukafika upande wa pili wa Kio, lakini siku iliyofuata tukafika Samo, na siku iliyofuata hiyo tukafika Mileto. 16 Kwa maana Paulo alikuwa ameamua kusafiri kupita Efeso,+ ili asitumie wakati wowote katika wilaya ya Asia; kwa maana alikuwa akifanya haraka afike Yerusalemu+ siku ya sherehe ya Pentekoste kama kwa vyovyote angeweza.

17 Hata hivyo, kutoka Mileto akatuma watu kwenda Efeso na kuwaita wanaume wazee+ wa hilo kutaniko waje. 18 Walipofika kwake akawaambia: “Ninyi mnajua vema jinsi tangu siku ya kwanza niliyokanyaga wilaya ya Asia+ nilivyokuwa pamoja nanyi wakati wote,+ 19 nikimtumikia+ Bwana nikiwa na unyenyekevu mkubwa zaidi wa akili+ na machozi na majaribu yaliyonipata kwa hila+ za Wayahudi; 20 wakati uleule sikuepuka kuwaambia ninyi lolote kati ya mambo yenye faida wala kuwafundisha+ ninyi hadharani na nyumba+ kwa nyumba. 21 Lakini nilitoa ushahidi+ kikamili kwa Wayahudi na Wagiriki pia juu ya toba+ kwa Mungu na imani katika Bwana wetu Yesu. 22 Na sasa, tazameni! nikiwa nimefungwa katika roho,+ ninafunga safari kwenda Yerusalemu, ijapokuwa sijui mambo yatakayonipata katika jiji hilo, 23 ila kwamba kutoka jiji mpaka jiji roho takatifu+ inatoa ushahidi kwangu kwa kurudiarudia inaposema kwamba vifungo na dhiki vinaningojea.+ 24 Hata hivyo, siifanyi nafsi yangu kuwa kitu chenye thamani sana kwangu,+ kama tu ningepata kumaliza mwendo+ wangu na huduma+ niliyopokea+ kutoka kwa Bwana Yesu, kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu.+

25 “Na sasa, tazameni! ninajua kwamba ninyi nyote ambao nilienda kati yenu nikihubiri juu ya ufalme hamtauona uso wangu tena. 26 Kwa sababu hiyo ninawaita ninyi kuona ushahidi leo hii kwamba mimi ni safi kutokana na damu+ ya watu wote, 27 kwa maana sikuepuka kuwaambia ninyi mashauri+ yote ya Mungu. 28 Jiangalieni+ ninyi wenyewe+ na kundi lote,+ ambalo roho takatifu imewaweka ninyi rasmi kuwa waangalizi+ kati yake, kulichunga kutaniko la Mungu,+ ambalo alilinunua kwa damu+ ya Mwana wake mwenyewe. 29 Ninajua kwamba baada ya kuondoka kwangu mbwa-mwitu+ wenye kukandamiza wataingia katikati yenu nao hawatalitendea kundi kwa wororo, 30 na kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka+ ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.+

31 “Kwa hiyo endeleeni kukesha, na kukumbuka akilini kwamba kwa miaka mitatu,+ usiku na mchana, sikuacha kumwonya+ kila mmoja kwa machozi. 32 Na sasa ninawaweka ninyi mikononi mwa Mungu+ na kwa neno la fadhili zake zisizostahiliwa, neno ambalo linaweza kuwajenga+ na kuwapa urithi kati ya wale wote waliotakaswa.+ 33 Sikutamani fedha au dhahabu au vazi la mtu.+ 34 Ninyi wenyewe mnajua kwamba mikono hii imehudumia mahitaji yangu+ na ya wale walio pamoja nami. 35 Nimewaonyesha ninyi wazi katika mambo yote kwamba kwa kufanya kazi+ kwa bidii hivyo ni lazima mwasaidie wale walio dhaifu,+ na lazima myakumbuke maneno ya Bwana Yesu, aliposema, ‘Kuna furaha zaidi katika kutoa+ kuliko ilivyo katika kupokea.’ ”

36 Alipokuwa amesema mambo haya, akapiga magoti+ pamoja nao wote na kusali. 37 Kwa kweli, wote wakalia sana, nao wakamwangukia Paulo shingoni+ na kumbusu+ kwa wororo, 38 kwa sababu waliumizwa hasa na neno alilosema kwamba hawangemwona uso+ wake tena. Basi wakaanza kumsindikiza+ mpaka kwenye mashua.

21 Sasa tulipokuwa tumejiondoa kwao na kusafiri baharini, tulikwenda kwa mwendo wa moja kwa moja tukaja mpaka Kosi, lakini siku iliyofuata tukaja mpaka Rode, na kutoka huko mpaka Patara. 2 Na tulipokuwa tumepata mashua iliyokuwa ikivuka kwenda Foinike, tukapanda ndani, tukasafiri kwenda zetu. 3 Baada ya kuja mahali tulipoweza kuona kisiwa cha Kipro+ tukakiacha nyuma upande wa kushoto, tukasafiri mpaka Siria,+ tukafika Tiro, kwa maana mashua ilipaswa ipakue shehena yake huko.+ 4 Baada ya kuwatafuta, tuliwapata wanafunzi na kukaa huko siku saba. Lakini kupitia roho+ wakarudiarudia kumwambia Paulo asikanyage Yerusalemu. 5 Kwa hiyo tulipokuwa tumekamilisha hizo siku, tukatoka na kuanza kwenda; lakini hao wote, pamoja na wanawake na watoto, wakatupeleka mpaka nje ya jiji. Tukapiga magoti+ pwani, tukasali 6 na kuagana,+ nasi tukapanda ndani ya mashua lakini wao wakarudi nyumbani kwao.

7 Ndipo tukakamilisha safari ya baharini kutoka Tiro tukafika Tolemai, nasi tukawasalimu akina ndugu na kukaa siku moja pamoja nao. 8 Siku iliyofuata tukaondoka tukafika Kaisaria,+ nasi tukaingia katika nyumba ya Filipo mweneza-injili, aliyekuwa mmoja wa wale watu saba,+ nasi tukakaa pamoja naye. 9 Mtu huyu alikuwa na binti wanne, mabikira, waliotoa unabii.+ 10 Lakini tulipokuwa tukikaa siku kadhaa, nabii fulani anayeitwa Agabo+ akashuka kutoka Yudea, 11 naye akaja mahali tulipokuwa na kuuchukua mshipi wa Paulo, akafunga miguu na mikono yake mwenyewe na kusema: “Hivi ndivyo inavyosema roho takatifu, ‘Mwanamume ambaye mshipi huu ni wake, Wayahudi watamfunga+ hivi katika Yerusalemu na kumtia+ mikononi mwa watu wa mataifa.’ ” 12 Sasa tuliposikia jambo hilo, sisi na pia watu wa mahali hapo tukaanza kumsihi asipande+ kwenda Yerusalemu. 13 Ndipo Paulo akajibu: “Mnafanya nini kwa kulia+ na kunifanya dhaifu moyoni?+ Muwe na hakika, niko tayari si kufungwa tu bali pia kufa+ Yerusalemu kwa ajili ya jina la Bwana Yesu.” 14 Alipokataa kushawishika, tukakubali kimyakimya maneno haya: “Mapenzi+ ya Yehova na yatendeke.”

15 Sasa baada ya siku hizo tukajitayarisha kwa ajili ya safari, tukaanza kupanda kwenda Yerusalemu.+ 16 Lakini wengine kati ya wanafunzi kutoka Kaisaria+ wakaenda pamoja nasi pia, ili kutuleta kwa mtu ambaye nyumbani mwake tulipaswa kukaribishwa, Mnasoni wa Kipro, mwanafunzi wa zamani. 17 Tulipoingia Yerusalemu,+ akina ndugu wakatukaribisha kwa furaha.+ 18 Lakini siku iliyofuata Paulo akaingia pamoja nasi kwa Yakobo;+ na wanaume wote wazee walikuwapo. 19 Naye akawasalimu na kuanza kusimulia+ kirefu juu ya mambo ambayo Mungu alifanya katikati ya mataifa kupitia kwa huduma yake.+

20 Baada ya kusikia jambo hilo wakaanza kumtukuza Mungu, nao wakamwambia: “Unaona, ndugu, jinsi kulivyo na maelfu mengi ya waamini walio kati ya Wayahudi; nao wote ni wenye bidii kuhusu Sheria.+ 21 Lakini wamesikia uvumi ukitolewa juu yako kwamba wewe umekuwa ukiwafundisha Wayahudi wote kati ya mataifa uasi-imani wa kumwacha Musa,+ ukiwaambia wasiwatahiri+ watoto wao wala kujiendesha katika desturi za kisherehe. 22 Basi, ni nini kinachopaswa kufanywa juu ya hilo? Kwa vyovyote vile watasikia umefika. 23 Kwa hiyo fanya jambo hili tunalokuambia: Tuna wanaume wanne wenye nadhiri juu yao wenyewe. 24 Wachukue watu hawa pamoja nawe+ ujitakase kisherehe pamoja nao na kuwagharimia,+ ili wapate kunyolewa+ vichwa vyao. Na kwa hiyo kila mtu atajua kwamba uvumi mwingi walioambiwa juu yako si kitu, bali kwamba unatembea kwa utaratibu, wewe mwenyewe pia ukishika Sheria.+ 25 Kwa habari ya wale waamini kutoka kati ya mataifa, tumetuma watu, tukitoa uamuzi wetu kwamba wanapaswa kujiepusha na vitu vilivyotolewa dhabihu kwa sanamu+ na pia damu+ na vitu vilivyonyongwa,+ na uasherati.”+

26 Ndipo Paulo akawachukua wanaume hao pamoja naye siku iliyofuata akajitakasa kisherehe pamoja nao+ na kuingia ndani ya hekalu, kutoa taarifa juu ya siku ambazo zingetimizwa+ kwa huo utakaso wa kisherehe, mpaka toleo+ litolewe kwa ajili ya kila mmoja wao.+

27 Sasa zile siku saba+ zilipokuwa karibu kumalizika, Wayahudi kutoka Asia walipomwona katika hekalu wakaanza kuuvuruga umati wote,+ nao wakamkamata, 28 wakipaaza sauti: “Wanaume wa Israeli, saidieni! Huyu ndiye mwanamume anayefundisha kila mtu kila mahali dhidi ya watu+ na Sheria na mahali hapa na, zaidi ya hayo, hata aliwaingiza Wagiriki katika hekalu naye amepatia unajisi mahali hapa patakatifu.”+ 29 Kwa maana hapo kwanza walikuwa wamemwona Trofimo+ Mwefeso katika jiji akiwa pamoja naye, lakini walikuwa wakiwazia Paulo alikuwa amemwingiza katika hekalu. 30 Na jiji lote likawa na mchafuko,+ na watu wakaanza kukimbia pamoja; nao wakamkamata Paulo wakamkokota nje ya hekalu.+ Na mara moja milango ikafungwa. 31 Na walipokuwa wakitafuta kumuua, kiongozi wa kikosi cha askari-jeshi akaletewa habari kwamba Yerusalemu lote lilikuwa katika mvurugo;+ 32 naye mara moja akachukua askari-jeshi na maofisa-jeshi na kuwakimbilia huko chini.+ Walipomwona kiongozi huyo wa kijeshi+ na askari-jeshi, wakaacha kumpiga Paulo.

33 Ndipo kiongozi wa kijeshi akaja karibu akamkamata na kutoa amri afungwe minyororo miwili;+ naye akaanza kuuliza huyo ni nani na alikuwa amefanya nini. 34 Lakini wengine katika umati wakaanza kupaaza sauti kuhusu jambo moja, na wengine kuhusu lingine.+ Kwa hiyo, kwa kuwa hangeweza kujua jambo lolote la hakika kwa sababu ya fujo hizo, akaamuru aletwe kwenye makao ya askari-jeshi.+ 35 Lakini alipofika juu ya ngazi, akachukuliwa na wale askari-jeshi kwa sababu ya jeuri ya umati; 36 kwa maana umati wa watu uliendelea kufuata, ukipaaza sauti: “Mwondolee mbali!”+

37 Na alipokuwa karibu kuingizwa katika makao ya askari-jeshi, Paulo akamwambia kiongozi wa kijeshi: “Je, ninaruhusiwa kukuambia jambo fulani?” Akasema: “Je, unaweza kusema Kigiriki? 38 Je, kwa kweli wewe si yule Mmisri ambaye kabla ya siku hizi alichochea uasi+ na kuwaongoza kuingia nyikani wale wanaume elfu nne wenye kutumia visu?” 39 Ndipo Paulo akasema: “Mimi, kwa kweli, ni Myahudi+ wa Tarso+ katika Kilikia, raia wa jiji ambalo si lenye kukosa umashuhuri. Kwa hiyo ninakuomba, uniruhusu niseme na watu hawa.” 40 Baada ya kutoa ruhusa, Paulo, akiwa amesimama juu ya ngazi, akawapungia+ watu mkono wake. Kulipokuwa na kimya kikubwa, akawahutubia kwa lugha ya Kiebrania,+ akisema:

22 “Wanaume, akina ndugu+ na akina baba, sikieni kujitetea+ kwangu mbele yenu sasa.” 2 (Basi, waliposikia alikuwa akisema nao katika lugha ya Kiebrania,+ wakakaa kimya hata zaidi, naye akasema:) 3 “Mimi ni Myahudi,+ aliyezaliwa katika Tarso ya Kilikia,+ lakini aliyeelimishwa katika jiji hili miguuni pa Gamalieli,+ nikiwa nimefundishwa kwa usahihi+ kabisa Sheria ya mababu, nikiwa mwenye bidii+ kuhusu Mungu kama vile ninyi nyote mlivyo leo hii. 4 Nami niliitesa Njia hii mpaka kifo,+ nikifunga na kutia magerezani+ wanaume na wanawake pia, 5 kama ambavyo kuhani mkuu na pia kusanyiko lote la wanaume wazee+ wanavyoweza kunitolea ushahidi. Kutoka kwao nilipata pia barua+ nizipeleke kwa akina ndugu katika Damasko, nami nilikuwa ninaenda kuwaleta wale waliokuwa huko pia mpaka Yerusalemu wakiwa wamefungwa ili waadhibiwe.

6 “Lakini nilipokuwa nikisafiri na kukaribia Damasko, karibu katikati ya mchana, kwa ghafula nuru kubwa kutoka mbinguni ikamulika kunizunguka,+ 7 nami nikaanguka chini na kusikia sauti ikiniambia, ‘Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa?’+ 8 Nikajibu, ‘Wewe ni nani, Bwana?’ Naye akaniambia, ‘Mimi ni Yesu Mnazareti, ambaye unatesa.’+ 9 Basi watu waliokuwa pamoja nami,+ kwa kweli, wakaiona nuru hiyo lakini hawakuisikia sauti ya mwenye kusema nami.+ 10 Ndipo nikasema, ‘Nitafanya nini,+ Bwana?’ Bwana akaniambia, ‘Simama, ondoka uende Damasko, na huko utaambiwa kila kitu ambacho umewekewa kufanya.’+ 11 Lakini kwa kuwa singeweza kuona kitu chochote kwa sababu ya utukufu wa nuru hiyo, nikafika Damasko, nikiwa ninaongozwa kwa mkono wa wale waliokuwa pamoja nami.+

12 “Basi Anania, mwanamume fulani mwenye kumheshimu Mungu kulingana na Sheria, mwenye kushuhudiwa vema+ na Wayahudi wote waliokuwa wakikaa huko, 13 akaja kwangu, akasimama kando yangu, akaniambia, ‘Sauli, ndugu, pata kuona tena!’+ Nami nikatazama juu kumwelekea saa ileile. 14 Akasema, ‘Mungu wa mababu+ zetu amekuchagua+ upate kujua mapenzi yake na kumwona+ yule Aliye mwadilifu+ na kuisikia sauti ya kinywa chake,+ 15 kwa sababu unapaswa kuwa shahidi kwa ajili yake kwa watu wote juu ya mambo ambayo umeona na kusikia.+ 16 Na sasa kwa nini unakawia? Simama, ubatizwe+ na uoshe+ dhambi zako kwa kuliitia jina lake.’+

17 “Lakini nilipokuwa nimerudi Yerusalemu+ na nikiwa ninasali hekaluni, nikapata njozi+ 18 na kumwona akiniambia, ‘Fanya upesi uondoke Yerusalemu haraka, kwa sababu hawatakubali+ ushahidi wako kunihusu.’ 19 Nami nikasema, ‘Bwana, wao wenyewe wanajua vema kwamba nilikuwa nikiwatia gerezani+ na kuwapiga viboko katika sinagogi moja baada ya lingine wale wenye kukuamini;+ 20 na wakati damu ya Stefano+ shahidi wako ilipokuwa ikimwagwa, mimi mwenyewe nilikuwa pia nimesimama kando nikikubaliana+ na jambo hilo na kuyalinda mavazi ya nje ya hao waliokuwa wakimuua.’ 21 Na bado akaniambia, ‘Ondoka uende, kwa sababu nitakutuma mbali sana kwa mataifa.’ ”+

22 Basi wakaendelea kumsikiliza mpaka kwenye neno hili, nao wakapaaza sauti zao, wakisema: “Mwondolee mbali mtu wa namna hiyo duniani, kwa maana yeye hakufaa kuishi!”+ 23 Na kwa sababu walikuwa wakipaaza sauti na kutupa mavazi yao ya nje huku na huku na kurusha mavumbi hewani,+ 24 yule kiongozi wa kijeshi akaagiza aingizwe katika makao ya askari-jeshi na kusema anapaswa kuhojiwa kwa kupigwa mijeledi, ili apate kujua kabisa ni kwa sababu gani walikuwa wakipaaza sauti+ juu yake kwa njia hii. 25 Lakini walipokuwa wamemnyoosha ili apigwe mijeledi, Paulo akamwambia ofisa-jeshi aliyekuwa amesimama hapo: “Je, ni halali kwa ninyi watu kumpiga mijeledi mtu ambaye ni Mroma+ na ambaye hajahukumiwa kuwa mwenye hatia?” 26 Basi, huyo ofisa-jeshi aliposikia jambo hilo, akaenda mpaka kwa kiongozi wa kijeshi na kueleza, akisema: “Unakusudia kufanya nini? Kwani, mtu huyu ni Mroma.” 27 Kwa hiyo kiongozi wa kijeshi akakaribia na kumwambia: “Niambie, Je, wewe ni Mroma?”+ Akasema: “Ndiyo.” 28 Kiongozi wa kijeshi akajibu: “Mimi nilinunua haki hizo za kuwa raia kwa pesa nyingi.” Paulo akasema: “Lakini mimi, hata nilizaliwa+ nazo.”

29 Kwa hiyo, mara moja watu waliokuwa karibu kumhoji kwa kumtesa wakaondoka kwake; na kiongozi wa kijeshi akaogopa alipohakikisha kwamba alikuwa Mroma+ na kwamba alikuwa amemfunga.

30 Kwa hiyo, siku iliyofuata, kwa kuwa alitaka kujua kwa hakika ni kwa nini hasa alikuwa akishtakiwa na Wayahudi, akamfungua na kuwaamuru wakuu wa makuhani na Sanhedrini yote wakusanyike. Naye akamleta Paulo chini na kumsimamisha katikati yao.+

23 Paulo akaikazia macho Sanhedrini, akasema: “Wanaume, akina ndugu, nimejiendesha mbele za Mungu kwa dhamiri+ iliyo safi kikamilifu mpaka leo hii.” 2 Ndipo kuhani mkuu Anania akawaagiza wale waliosimama kando yake wampige+ kinywani. 3 Ndipo Paulo akamwambia: “Mungu atakupiga wewe, ewe ukuta uliopakwa chokaa.+ Je, wakati uleule mmoja unaketi kunihukumu kupatana na Sheria+ na, kwa kuvunja Sheria,+ unaamuru nipigwe?” 4 Wale waliosimama kando wakasema: “Je, wewe unamtukana kuhani mkuu wa Mungu?” 5 Na Paulo akasema: “Akina ndugu, sikujua yeye ni kuhani mkuu. Kwa maana imeandikwa, ‘Usiseme vibaya juu ya mtawala wa watu wako.’ ”+

6 Sasa Paulo alipojua kwamba sehemu moja ilikuwa ya Masadukayo+ lakini ile nyingine ya Mafarisayo, akapaaza sauti katika Sanhedrini hiyo: “Wanaume, akina ndugu, mimi ni Farisayo,+ mwana wa Mafarisayo. Ninahukumiwa+ juu ya tumaini la ufufuo+ wa wafu.” 7 Kwa sababu alisema jambo hilo, mtengano+ ukatokea kati ya Mafarisayo na Masadukayo, na umati ukagawanyika. 8 Kwa maana Masadukayo+ husema hakuna ufufuo+ wala malaika wala roho, lakini Mafarisayo huyatangaza yote hadharani. 9 Kwa hiyo watu wakaanza kupiga mayowe+ kwa sauti kubwa, na wengine kati ya waandishi wa chama cha Mafarisayo wakasimama na kuanza kushindana vikali, wakisema: “Sisi hatuoni kosa lolote katika mtu huyu;+ lakini ikiwa roho au malaika alisema naye,+ —.” 10 Basi mtengano ulipokuwa mkubwa, kiongozi wa kijeshi akaogopa kwamba wangemrarua Paulo vipande-vipande, naye akaamuru jeshi la askari+ lishuke liende kumnyakua kutoka katikati yao na kumleta ndani ya makao ya askari-jeshi.+

11 Lakini usiku uliofuata Bwana akasimama kando yake+ na kusema: “Jipe moyo!+ Kwa maana kama vile ambavyo umekuwa ukitoa ushahidi+ kamili katika Yerusalemu juu ya mambo yanayonihusu, vivyo hivyo utatoa ushahidi katika Roma pia.”+

12 Sasa kulipokuwa mchana, Wayahudi wakafanya hila+ na kujifunga wenyewe kwa laana,+ wakisema hawangekula wala kunywa mpaka wawe wamemuua Paulo.+ 13 Kulikuwa na zaidi ya watu 40 waliofanya hila hiyo iliyofungwa kwa kiapo; 14 nao wakaenda kwa wakuu+ wa makuhani na wanaume wazee na kusema: “Sisi tumejifunga wenyewe chini ya laana kwa uzito kutoonja chakula mpaka tuwe tumemuua Paulo. 15 Kwa hiyo, basi, ninyi pamoja na Sanhedrini mfanyeni kiongozi wa kijeshi aelewe ni kwa nini anapaswa kumshusha chini kwenu kana kwamba mnakusudia kuhakikisha kwa usahihi zaidi mambo yanayomhusu.+ Lakini kabla hajafika karibu tutakuwa tayari kumuua.”+

16 Hata hivyo, mwana wa dada ya Paulo akasikia juu ya kuvizia kwao,+ naye akaja na kuingia katika makao ya askari-jeshi hao akamweleza Paulo jambo hilo. 17 Basi Paulo akamwita mmoja wa maofisa-jeshi na kusema: “Mpeleke kijana huyu kwa kiongozi wa kijeshi, kwa maana ana jambo fulani la kumweleza.” 18 Kwa hiyo mtu huyu akamchukua na kumpeleka kwa kiongozi wa kijeshi na kusema: “Mfungwa Paulo aliniita na kuniomba nimlete kijana huyu kwako, kwa kuwa ana jambo la kukuambia.” 19 Kiongozi wa kijeshi akamshika+ mkono, akaondoka, na kuanza kumuuliza faraghani: “Unataka kuniambia nini?” 20 Akasema: “Wayahudi wamepatana kukuomba umshushe Paulo kwenye Sanhedrini kesho kana kwamba wanakusudia kujua jambo fulani kwa usahihi zaidi juu yake.+ 21 Zaidi ya mambo yote, usiwaache wakushawishi, kwa maana wanaume wao zaidi ya 40 wanamvizia,+ nao wamejifunga wenyewe kwa laana kutokula wala kunywa mpaka wawe wamemuua;+ nao sasa wako tayari, wakingojea ahadi kutoka kwako.” 22 Kwa hiyo huyo kiongozi wa kijeshi akamwacha huyo kijana aende baada ya kumwagiza: “Usipayuke-payuke kwa yeyote kwamba umenieleza mambo hayo.”

23 Naye akawaita watu fulani wawili kati ya maofisa-jeshi na kusema: “Tayarisheni askari-jeshi 200 ili waende moja kwa moja mpaka Kaisaria, pia wapanda-farasi 70 na watu 200 wachukua-mikuki, saa tatu ya usiku. 24 Pia, andaeni wanyama wa kubeba mizigo ili wampandishe Paulo na kumpeleka salama kwa Feliksi gavana.” 25 Naye akaandika barua ya namna hii:

26 “Klaudio Lisia kwa mtukufu, Gavana Feliksi:+ Salamu! 27 Mwanamume huyu alikamatwa na Wayahudi nao walikuwa karibu kumuua, lakini nikaja ghafula nikiwa pamoja na jeshi la askari na kumwokoa,+ kwa sababu nilipata kujua kwamba yeye ni Mroma.+ 28 Nami nikitaka kuhakikisha sababu waliyokuwa wakimshtakia, nikamleta ndani ya Sanhedrini yao.+ 29 Niliona ameshtakiwa juu ya maswali ya Sheria yao,+ lakini hajashtakiwa hata jambo moja la kustahili kifo au vifungo.+ 30 Lakini kwa sababu hila+ itakayofanywa juu ya mwanamume huyu imefunuliwa kwangu, ninamtuma kwako mara moja, na kuwaamuru washtaki wamshtaki mbele yako.”+

31 Kwa hiyo askari-jeshi+ hao wakamchukua Paulo kulingana na walivyoagizwa wakamleta wakati wa usiku mpaka Antipatri. 32 Siku iliyofuata wakaruhusu wapanda-farasi waende pamoja naye, nao wakarudi kwenye makao ya askari-jeshi. 33 Hao wapanda-farasi wakaingia katika Kaisaria+ na kumkabidhi gavana hiyo barua na pia wakamleta Paulo mbele yake. 34 Basi akaisoma na kuuliza alikuwa ametoka jimbo gani, akapata kujua hakika+ kwamba alikuwa ametoka Kilikia.+ 35 “Nitasikia kesi yako vilivyo,” akasema, “washtaki wako watakapofika pia.”+ Naye akaamuru kwamba awekwe chini ya ulinzi katika jumba la kimaliki la Herode.

24 Siku tano baadaye kuhani mkuu Anania+ akashuka pamoja na wanaume fulani wazee na msemaji wa hadharani, Tertulo, nao wakamweleza+ gavana+ juu ya Paulo. 2 Alipoitwa, Tertulo akaanza kumshtaki, akisema:

“Kwa kuwa tunaonea shangwe amani+ kubwa kupitia kwako na kwamba marekebisho yanatokea katika taifa hili kupitia ufikirio wako wa kimbele, 3 nyakati zote na pia mahali pote tunapokea mambo hayo, Ewe Mtukufu+ Feliksi, kwa shukrani zilizo kubwa zaidi. 4 Lakini ili nisikuzuie zaidi, ninakuomba utusikie kwa ufupi kwa fadhili zako. 5 Kwa maana tumemwona mwanamume huyu kuwa mtu msumbufu+ na mwenye kufanya uchochezi wa uasi+ kati ya Wayahudi wote katika dunia yote inayokaliwa na kuwa kiongozi mkuu wa madhehebu ya Wanazareti,+ 6 ambaye pia alijaribu kulichafua hekalu+ na ambaye tulimkamata. 7 —— 8 Kutoka kwake wewe mwenyewe unaweza kugundua kwa kumhoji juu ya mambo haya yote ambayo sisi tunamshtaki.”

9 Ndipo Wayahudi pia wakajiunga katika shambulio hilo, wakisisitiza kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo. 10 Na Paulo, wakati gavana alipomtolea ishara aseme, akajibu:

“Kwa kujua vema kwamba wewe umekuwa mwamuzi wa taifa hili kwa miaka mingi, mimi ninasema kwa utayari katika kujitetea+ juu ya mambo yanayonihusu mimi mwenyewe, 11 kwa kuwa wewe unaweza kugundua kwamba kwangu mimi haijawa zaidi ya siku kumi na mbili tangu nilipopanda kwenda kuabudu+ katika Yerusalemu; 12 nao hawakuniona katika hekalu+ nikibishana na mtu yeyote wala nikifanya kikundi chenye ghasia+ kikimbie pamoja, ama katika masinagogi ama kotekote katika jiji. 13 Wala hawawezi kukuthibitishia+ mambo wanayonishtaki sasa hivi. 14 Lakini ninakiri jambo hili kwako, kwamba, kulingana na ile njia wanayoiita ‘madhehebu,’ kwa namna hii mimi ninatoa utumishi mtakatifu kwa Mungu wa mababu zangu,+ kwa kuwa ninaamini mambo yote yaliyo katika Sheria+ na kuandikwa katika Manabii; 15 nami nina tumaini+ kwa Mungu, tumaini ambalo watu hawa pia wanalo, kwamba kutakuwa na ufufuo+ wa waadilifu+ na wasio waadilifu+ pia. 16 Katika habari hii, kwa kweli, ninajizoeza mwenyewe sikuzote kudhamiria+ kutomkosea Mungu na wanadamu. 17 Kwa hiyo baada ya miaka kadhaa nilifika kuleta zawadi za rehema kwa taifa langu, na matoleo.+ 18 Nilipokuwa nikishughulikia mambo haya wakanikuta nikiwa nimetakaswa kisherehe katika hekalu,+ lakini nikiwa bila umati wala fujo. Lakini kulikuwa na Wayahudi fulani kutoka wilaya ya Asia, 19 ambao wanapaswa kuwapo mbele yako na kunishtaki ikiwa wana jambo lolote juu yangu.+ 20 Au, acha watu walio hapa wajisemee wenyewe ni kosa gani waliloona nilipokuwa nimesimama mbele ya Sanhedrini, 21 ila kwa habari ya neno hili moja nililopaaza sauti nikiwa nimesimama kati yao, ‘Mimi ninahukumiwa leo mbele yenu juu ya ufufuo wa wafu!’ ”+

22 Hata hivyo, Feliksi,+ akijua kwa usahihi kabisa mambo yanayoihusu Njia+ hii, akaahirisha kesi ya watu hao na kusema: “Wakati wowote Lisia+ kiongozi wa kijeshi atakapokuja, nitaamua mambo haya yanayowahusu ninyi.” 23 Naye akamwagiza ofisa-jeshi kwamba mtu huyo atunzwe na awe na starehe fulani ya kizuizini, na kwamba asimkataze yeyote kati ya watu wake kumhudumia.+

24 Siku kadhaa baadaye Feliksi+ akafika pamoja na Drusila mke wake, aliyekuwa Myahudi,+ naye akatuma watu kumwita Paulo na kumsikiliza juu ya imani katika Kristo Yesu.+ 25 Lakini alipokuwa akiongea juu ya uadilifu+ na kujizuia+ na hukumu+ itakayokuja, Feliksi akaogopa na kujibu: “Kwa wakati huu wa sasa ondoka uende, lakini nitakapopata wakati unaofaa nitakuita tena.” 26 Ingawa hivyo, wakati huohuo, alikuwa akitumaini Paulo ampe pesa.+ Kwa ajili ya hilo akamwita mara nyingi hata zaidi na akawa akiongea naye.+ 27 Lakini, miaka miwili ilipokuwa imepita, nafasi ya Feliksi ilichukuliwa na Porkio Festo; na kwa sababu Feliksi alitamani kupata kibali+ cha Wayahudi, akamwacha Paulo akiwa amefungwa.

25 Kwa hiyo Festo, baada ya kuingia+ katika cheo cha serikali ya jimbo, siku tatu baadaye alipanda kwenda Yerusalemu kutoka Kaisaria;+ 2 na wakuu wa makuhani na watu walio wakuu kati ya Wayahudi wakamweleza+ mashtaka juu ya Paulo. Basi wakaanza kumsihi, 3 wakijiombea kibali dhidi ya mtu huyo ili amwite aje mpaka Yerusalemu, kwa kuwa walikuwa wakivizia+ ili kumuua barabarani. 4 Hata hivyo, Festo akajibu kwamba Paulo alipaswa kulindwa katika Kaisaria na kwamba yeye mwenyewe angeenda huko hivi karibuni. 5 “Kwa sababu hiyo acheni wale walio na mamlaka kati yenu,” akasema, “washuke pamoja nami na kumshtaki,+ ikiwa kuna jambo lolote lisilofaa juu ya mwanamume huyo.”

6 Kwa hiyo alipokuwa amekaa siku zisizozidi nane au kumi kati yao, akashuka kwenda Kaisaria, na siku iliyofuata akaketi juu ya kiti cha hukumu+ na kuamuru Paulo aingizwe ndani. 7 Alipofika, Wayahudi waliokuwa wameshuka kutoka Yerusalemu wakasimama kumzunguka huku na huku, wakileta juu yake mashtaka+ mengi na mazito ambayo hawakuweza kuthibitisha.

8 Lakini Paulo akasema kwa kujitetea: “Sijatenda dhambi yoyote juu ya Sheria ya Wayahudi wala juu ya hekalu wala juu ya Kaisari.”+ 9 Festo, akitamani kupata kibali+ cha Wayahudi, akasema kwa kumjibu Paulo: “Je, wewe ungetaka kupanda kwenda Yerusalemu uhukumiwe huko mbele yangu kuhusu mambo haya?”+ 10 Lakini Paulo akasema: “Mimi nimesimama mbele ya kiti cha hukumu cha Kaisari,+ ambapo ninapaswa kuhukumiwa. Sijawatendea Wayahudi kosa,+ kama vile wewe pia unavyogundua vema kabisa. 11 Ikiwa, kwa upande mmoja, mimi ni mkosaji+ kwa kweli na nimefanya jambo lolote linalostahili kifo,+ sikatai kufa; ikiwa, kwa upande mwingine, hakuna hata moja la mambo hayo ambalo watu hawa wananishtakia, hakuna mtu anayeweza kunikabidhi kwao ili kupata kibali. Ninakata rufani kwa Kaisari!”+ 12 Ndipo Festo, baada ya kusema na kusanyiko la washauri, akajibu: “Umekata rufani kwa Kaisari; utaenda kwa Kaisari.”

13 Basi siku kadhaa zilipokuwa zimepita, Agripa mfalme na Bernike wakafika Kaisaria kwa ziara ya kumsalimu Festo. 14 Kwa kuwa walikuwa wakikaa siku kadhaa huko, Festo akaweka mbele ya mfalme mambo yanayomhusu Paulo, akisema:

“Kuna mwanamume fulani ambaye Feliksi alimwacha akiwa mfungwa, 15 na nilipokuwa Yerusalemu wakuu wa makuhani na wanaume wazee wa Wayahudi walileta habari+ juu yake, wakiomba hukumu ya adhabu juu yake. 16 Lakini nikawajibu kwamba si utaratibu wa Kiroma kukabidhi mtu yeyote ili kupata kibali kabla ya mtu huyo aliyeshtakiwa kukutana uso kwa uso na washtaki+ wake na kupata nafasi ya kujitetea kuhusu malalamishi. 17 Kwa hiyo walipokuja pamoja hapa, sikukawia, bali siku iliyofuata niliketi juu ya kiti cha hukumu na kuamuru mwanamume huyo aingizwe ndani. 18 Waliposimama, washtaki hawakutokeza shtaka+ juu ya mambo maovu niliyokuwa nimedhani kumhusu. 19 Walikuwa tu na mabishano fulani pamoja naye kuhusu ibada+ yao wenyewe ya mungu na kuhusu mtu fulani anayeitwa Yesu aliyekuwa amekufa lakini ambaye Paulo alikuwa akisisitiza kwamba alikuwa hai.+ 20 Kwa hiyo, nikiwa nimefadhaishwa na bishano juu ya mambo haya, niliendelea kuuliza kama angependa kwenda mpaka Yerusalemu na huko akahukumiwe kuhusu mambo haya.+ 21 Lakini Paulo alipokata rufani+ awekwe kwa ajili ya uamuzi wa Mheshimiwa, nikaamuru awekwe mpaka nimtume kwa Kaisari.”

22 Hapo Agripa akamwambia Festo: “Mimi mwenyewe ningependa pia kumsikia mtu huyo.”+ “Kesho,” akasema, “Utamsikia.” 23 Kwa hiyo, siku iliyofuata, Agripa na Bernike wakaja kwa fahari+ nyingi na kuingia katika chumba cha baraza pamoja na viongozi wa kijeshi na vilevile wanaume waheshimiwa katika jiji, na Festo alipotoa amri, Paulo akaingizwa ndani. 24 Naye Festo akasema: “Mfalme Agripa na ninyi wanaume wote mliopo pamoja nasi, ninyi mnaona mtu huyu ambaye kuhusu yeye umati wote wa Wayahudi ukiwa pamoja umepeleka ombi kwangu katika Yerusalemu na hapa pia, ukipaaza sauti kwamba hapaswi kuishi tena kamwe.+ 25 Lakini mimi nikaona hakuwa amefanya jambo lolote linalostahili kifo.+ Kwa hiyo mwanamume huyu mwenyewe alipokata rufani+ kwa Mheshimiwa, niliamua kumpeleka. 26 Lakini kuhusu yeye sina jambo hakika la kumwandikia Bwana wangu. Kwa hiyo nikamleta mbele yenu, na hasa mbele yako wewe, Mfalme Agripa, ili, baada ya kumhoji kihukumu,+ nipate jambo fulani la kuandika. 27 Kwa maana linaonekana kuwa jambo lisilo la akili kwangu kumpeleka mfungwa bila kuonyesha mashtaka juu yake.”

26 Agripa+ akamwambia Paulo: “Unaruhusiwa kujitetea.” Ndipo Paulo akanyoosha mkono+ wake na kuanza kujitetea:+

2 “Kuhusu mambo yote ninayoshtakiwa+ na Wayahudi, Mfalme Agripa, ninajihesabu mwenyewe kuwa mwenye furaha kwamba ninajitetea mbele yako leo, 3 hasa kwa kuwa wewe una ujuzi juu ya desturi+ zote na vilevile mabishano kati ya Wayahudi. Kwa hiyo ninakuomba unisikie kwa subira.

4 “Kwa kweli, juu ya maisha+ ya tangu ujana na kuendelea ambayo niliishi tangu mwanzo kati ya taifa langu na katika Yerusalemu, Wayahudi wote 5 ambao walinifahamu tangu mwanzo wanajua, kama tu wangetaka kutoa ushahidi, kwamba kulingana na usahihi kabisa wa madhehebu+ ya namna yetu ya ibada mimi niliishi nikiwa Farisayo.+ 6 Lakini sasa kwa sababu ya tumaini+ la ahadi+ iliyotolewa na Mungu kwa mababu zetu nimeitwa kwenye hukumu; 7 lakini makabila yetu kumi na mawili yanatumaini kufikia utimizo wa ahadi hii kwa kumtolea utumishi mtakatifu kwa juhudi nyingi usiku na mchana.+ Kuhusu tumaini hili ninashtakiwa+ na Wayahudi, Ewe mfalme.

8 “Kwa nini mnaamua kwamba ni jambo lisiloaminika kwamba Mungu hufufua wafu?+ 9 Mimi, kwa kweli nilifikiri ndani yangu mwenyewe kwamba ninapaswa kufanya matendo mengi ya upinzani juu ya jina la Yesu Mnazareti; 10 ambayo, kwa kweli, niliyafanya katika Yerusalemu, na wengi kati ya watakatifu niliwafunga gerezani,+ kwa kuwa nilikuwa nimepokea mamlaka kutoka kwa wakuu wa makuhani;+ na walipokuwa wanapaswa kuuawa, mimi nilipiga kura yangu dhidi yao. 11 Na kwa kuwaadhibu nyakati nyingi katika masinagogi+ yote nilijaribu kuwalazimisha wakane imani yao; na kwa kuwa nilikuwa nimejawa na wazimu kupita kiasi juu yao, nilifikia hatua ya kuwatesa hata katika majiji ya nje.

12 “Katikati ya jitihada hizo nilipokuwa nikisafiri kwenda Damasko+ nikiwa na mamlaka na utume kutoka kwa wakuu wa makuhani, 13 katikati ya mchana niliona barabarani, Ee mfalme, nuru inayopita wangavu wa jua ikimulika kutoka mbinguni kunizunguka na kuwazunguka wale waliokuwa wakisafiri pamoja nami.+ 14 Na sisi sote tulipokuwa tumeanguka chini nikasikia sauti ikiniambia katika lugha ya Kiebrania, ‘Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa? Kuendelea kuipiga teke michokoo hufanya iwe vigumu kwako.’+ 15 Lakini nikasema, ‘Wewe ni nani, Bwana?’ Naye Bwana akasema, ‘Mimi ni Yesu, ambaye unatesa.+ 16 Hata hivyo, inuka usimame kwa miguu yako.+ Kwa maana nimejionyesha kwako kwa sababu hii, ili nikuchague wewe uwe mtumishi na shahidi+ wa mambo ambayo umeona na pia mambo nitakayokuonyesha juu yangu; 17 huku mimi nikikukomboa kutoka kwa watu hawa na kutoka katika mataifa, ambao kwao ninakutuma wewe,+ 18 kufungua macho+ yao, kuwageuza kutoka katika giza+ kuingia katika nuru+ na kutoka katika mamlaka ya Shetani+ na kumgeukia Mungu, kusudi wapokee msamaha wa dhambi+ na urithi+ kati ya wale waliotakaswa+ kwa imani yao kwangu.’

19 “Kwa sababu hii, Mfalme Agripa, mimi sikukosa kutii maono hayo ya kimbingu,+ 20 lakini kwa wale walio katika Damasko+ kwanza na pia kwa wale walio katika Yerusalemu,+ na juu ya nchi yote ya Yudea, na kwa mataifa+ nilienda nikiuleta ujumbe kwamba wao wanapaswa kutubu na kumgeukia Mungu kwa kufanya matendo yanayostahili toba.+ 21 Kwa sababu ya mambo haya Wayahudi walinikamata katika hekalu na kujaribu kuniua.+ 22 Hata hivyo, kwa sababu nimeupata msaada+ kutoka kwa Mungu ninaendelea mpaka leo kutoa ushahidi kwa wadogo na wakubwa pia, lakini bila kusema lolote ila mambo ambayo Manabii+ na vilevile Musa+ walisema yatatukia, 23 kwamba Kristo angeteseka+ na, akiwa wa kwanza kufufuliwa+ kutoka kwa wafu, angetangaza nuru+ kwa watu hawa na pia kwa mataifa.”+

24 Sasa alipokuwa akisema mambo haya kwa kujitetea, Festo akasema kwa sauti kubwa: “Unashikwa na wazimu,+ Paulo! Kusoma kwingi kunakufanya uwe na wazimu!” 25 Lakini Paulo akasema: “Mimi sishikwi na wazimu, ewe Mtukufu Festo, bali ninasema maneno ya kweli na ya utimamu wa akili. 26 Kwa kweli, mfalme ambaye ninasema naye kwa uhuru wa kusema anajua vema juu ya mambo haya; kwa maana ninasadiki kwamba hakuna hata moja kati ya mambo haya ambalo hajui, kwa maana jambo hili halijafanywa pembeni.+ 27 Je, wewe, Mfalme Agripa, unawaamini Manabii? Ninajua unawaamini.”+ 28 Lakini Agripa akamwambia Paulo: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.” 29 Ndipo Paulo akasema: “Kama ingekuwa kwa muda mfupi au kwa muda mrefu mimi ningetaka kwa Mungu kwamba si wewe tu bali pia wote wanaonisikia leo wapate kuwa watu wa namna niliyo mimi, ila tu bila vifungo hivi.”

30 Naye mfalme akasimama na pia gavana na Bernike na watu walioketi pamoja nao. 31 Lakini walipokuwa wakiondoka wakaanza kuongea wao kwa wao, wakisema: “Mtu huyu hafanyi lolote linalostahili kifo+ au vifungo.” 32 Zaidi ya hayo, Agripa akamwambia Festo: “Mtu huyu angaliweza kufunguliwa kama hakuwa amekata rufani+ kwa Kaisari.”

27 Basi kwa kuwa iliamuliwa tusafiri kwenda Italia,+ walikuwa wakikabidhi Paulo na pia wafungwa fulani wengine kwa ofisa-jeshi anayeitwa Yulio wa kikosi cha Augusto. 2 Tukapanda ndani ya mashua kutoka Adramitiamu, iliyokuwa karibu kusafiri mpaka kandokando ya pwani ya wilaya ya Asia, tukasafiri kwa mashua, naye Aristarko+ Mmakedonia kutoka Thesalonike alikuwa pamoja nasi. 3 Na siku iliyofuata tukashuka mpaka Sidoni, na Yulio akamtendea Paulo kwa fadhili za kibinadamu+ na kumruhusu aende kwa rafiki zake na kutunzwa nao.+

4 Tulipotoka huko tukasafiri chini ya Kipro, kwa sababu pepo zilikuwa zikitukabili; 5 nasi tukaendesha kupitia bahari kuu kandokando ya Kilikia na Pamfilia na kuegesha bandarini kule Mira katika Likia. 6 Lakini huko ofisa-jeshi akapata mashua kutoka Aleksandria+ iliyokuwa ikisafiri kwenda Italia, naye akatupandisha chomboni. 7 Ndipo, baada ya kusafiri kwa mashua polepole kwa siku kadhaa na kufika Kinido kwa shida, kwa sababu upepo haukuturuhusu tuendelee mbele, tukasafiri chini ya Krete katika Salmone, 8 tukapita kandokando ya pwani yake kwa shida tukafika mahali fulani panapoitwa Bandari Nzuri, ambapo jiji Lasea lilikuwa karibu na hapo.

9 Kwa kuwa muda mrefu ulikuwa umepita na kufikia sasa ilikuwa hatari kusafiri kwa sababu hata kufunga kwa siku ya upatanisho+ kulikuwa tayari kumepita, Paulo alitoa pendekezo, 10 akiwaambia: “Ninaona kwamba safari itakuwa na madhara na hasara kubwa si ya shehena na mashua tu bali pia ya nafsi zetu.”+ 11 Hata hivyo, ofisa-jeshi akawa anamsikiliza nahodha na mwenye meli badala ya mambo yaliyosemwa na Paulo. 12 Sasa kwa kuwa bandari hiyo haikufaa kukaa wakati wa majira ya baridi kali, walio wengi wakakata shauri kusafiri kutoka hapo, ili kuona kama wangeweza kwa njia fulani kufaulu kufika Feniki ili kukaa huko wakati wa majira ya baridi kali, ambayo ni bandari ya Krete inayofunguka kuelekea kaskazini-mashariki na kuelekea kusini-mashariki.

13 Zaidi ya hayo, upepo wa kusini ulipovuma kwa utulivu, walifikiri walikuwa wamefikia kusudi lao, nao wakang’oa nanga na kuanza kufuata pwani karibu na pwani ya Krete. 14 Hata hivyo, baada ya muda usiokuwa mrefu, upepo wenye tufani+ unaoitwa Euroakilo ukavuma kasi juu yake. 15 Kwa kuwa mashua ilishikwa na upepo wenye nguvu nayo haikuweza kushindana na upepo huo, tukaiachilia, nao ukatuchukua. 16 Basi tukasafiri upesi chini ya kisiwa fulani kidogo kinachoitwa Kauda, na bado ilikuwa vigumu kuiongoza kikamili mashua+ ndogo kwenye tezi. 17 Lakini baada ya kuiingiza ndani wakaanza kutumia misaada ili kuikaza mashua chini; nao wakiogopa kupanda mwamba katika Sirti, wakashusha vifaa vya kuendeshea na hivyo wakachukuliwa. 18 Lakini kwa sababu tulikuwa tukirushwarushwa kwa nguvu nyingi na tufani hiyo, siku iliyofuata tukaanza kupunguza uzito+ wa meli; 19 na siku ya tatu, kwa mikono yao wenyewe, wakatupa ayari za mashua hiyo.

20 Basi, wakati ambapo jua wala nyota hazikuonekana kwa siku nyingi, nayo tufani+ iliyokuwa juu yetu ikiwa si ndogo, mwishowe tukaanza kukata tumaini la kuokolewa. 21 Na baada ya kujiepusha na chakula kwa muda mrefu, Paulo akasimama katikati yao+ na kusema: “Mlipaswa kufuata shauri langu na kutosafiri katika bahari kutoka Krete na hivyo mwepuke kupatwa na madhara na hasara hii.+ 22 Hata hivyo, sasa ninapendekeza mchangamke, kwa maana hakuna nafsi kati yenu itakayopotea, mashua tu ndiyo itakayopotea. 23 Kwa maana usiku huu malaika+ wa Mungu ambaye mimi ni mali yake na ambaye mimi ninamtolea utumishi mtakatifu, alisimama karibu nami,+ 24 akisema, ‘Usiogope, Paulo. Utasimama mbele ya Kaisari,+ na, tazama! Mungu amekupa wale wote wanaosafiri pamoja nawe.’ 25 Kwa hiyo changamkeni; kwa maana ninamwamini Mungu+ kwamba itakuwa kama vile ambavyo nimeambiwa. 26 Hata hivyo, lazima tutupwe pwani juu ya kisiwa fulani.”+

27 Sasa usiku wa kumi na nne ulipofika nasi tukawa tukirushwa huku na huku katika bahari ya Adria, katikati ya usiku mabaharia wakaanza kudhani walikuwa wakikaribia nchi fulani. 28 Nao wakapima kina kwa bildi na kupata kuwa ni pima 20; kwa hiyo wakaendelea mbele umbali mfupi na wakatia bildi tena na kupata kuwa ni pima 15. 29 Na kwa sababu ya kuogopa kwamba tungeweza kutupwa mahali fulani juu ya miamba, wakatupa nanga nne kutoka kwenye tezi na kuanza kutamani kupambazuke. 30 Lakini mabaharia walipoanza kutafuta kukimbia katika mashua na kushusha mashua ndogo ndani ya bahari kwa kusingizia kuwa walikusudia kuzishusha nanga kutoka kwenye omo, 31 Paulo akamwambia ofisa-jeshi na askari-jeshi: “Watu hawa wasipobaki katika mashua, ninyi hamwezi kuokolewa.”+ 32 Ndipo askari-jeshi wakakata kamba za mashua+ ndogo na kuiacha ianguke.

33 Sasa karibu na mapambazuko Paulo akaanza kuwatia moyo wote wale chakula, akisema: “Leo ni siku ya kumi na nne ambayo mmekuwa mkikesha na kukaa bila chakula, mkiwa hamjala chochote. 34 Kwa hiyo ninawatia moyo mle chakula, kwa ajili ya usalama wenu; kwa maana hata unywele+ mmoja wa kichwa cha mmoja kati yenu hautaangamia.” 35 Baada ya kusema jambo hilo, pia akachukua mkate, akamshukuru+ Mungu mbele yao wote akaumega na kuanza kula. 36 Kwa hiyo wote wakachangamka na kuanza kula chakula wao wenyewe. 37 Basi, sote pamoja, sisi nafsi tuliomo ndani ya mashua tulikuwa 276. 38 Walipokuwa wameshiba chakula, wakaanza kupunguza uzito+ wa mashua kwa kutupa ngano baharini.

39 Mwishowe kulipopambazuka, hawakuweza kuitambua nchi hiyo lakini walikuwa wakiangalia ghuba fulani yenye pwani, na hapo ndipo walipoazimia, ikiwa wangeweza, kuipeleka mashua pwani.+ 40 Kwa hiyo, wakizikata nanga, wakaziacha zianguke ndani ya bahari, wakati huohuo wakifungua amari za makasia ya mtambo wa usukani na, baada ya kutweka tanga la mbele kwenye upepo, wakaenda pwani. 41 Walipotua juu ya fungu la mchanga lililorundikwa na bahari pande zote mbili, wakaiendesha meli juu ya mwamba na omo ikakwama na kukaa bila kuondoleka, lakini tezi likaanza kuvunjika vipande-vipande kwa nguvu nyingi.+ 42 Ndipo askari-jeshi wakaazimia kuwaua wafungwa, ili yeyote asiogelee na kutoroka. 43 Lakini ofisa-jeshi akataka kumpitisha Paulo akiwa salama naye akawazuilia wasitimize kusudi lao. Naye akawaamuru wale ambao wangeweza kuogelea wajitupe baharini na kufika kwenye nchi kavu kwanza, 44 na wale wengine wafanye hivyo, wengine wakiwa juu ya mbao na wengine juu ya vitu fulani kutoka katika mashua. Na hivyo ikawa kwamba wote wakafika salama kwenye nchi kavu.+

28 Na tulipokuwa tumefika mahali salama, tukapata habari kwamba kisiwa hicho kilikuwa kikiitwa Malta.+ 2 Na watu hao wenye kusema lugha ya kigeni wakatuonyesha fadhili+ za kibinadamu zisizo za kawaida, kwa maana waliwasha moto na kutukaribisha sote na kutupa msaada kwa sababu ya mvua iliyokuwa ikinyesha na kwa sababu ya baridi.+ 3 Lakini Paulo alipokusanya tita la kuni na kuliweka juu ya moto, nyoka-kipiri akatoka kwa sababu ya joto na kujifunga kwenye mkono wake. 4 Watu hao wenye kusema lugha ya kigeni walipoona huyo kiumbe mwenye sumu akining’inia kwenye mkono wake, wakaanza kuambiana: “Hakika mtu huyu ni muuaji, na ingawa alifika mahali salama kutoka baharini, haki yenye kudai kisasi haikumruhusu aendelee kuishi.” 5 Hata hivyo, akamkung’uta kiumbe huyo mwenye sumu na kumtupa ndani ya moto, naye hakupatwa na dhara.+ 6 Lakini wao walikuwa wakitarajia atavimba kwa sababu ya mwasho au kwa ghafula aanguke na kufa. Baada ya kungojea kwa muda mrefu na kuona kwamba hakuna jambo lolote baya lililompata, wakabadili maoni yao na kuanza kusema kwamba yeye ni mungu.+

7 Sasa katika ujirani wa mahali hapo mkuu wa kisiwa hicho, anayeitwa Publio, alikuwa na mashamba; naye akatukaribisha na kutupokea kwa hisani kwa siku tatu. 8 Lakini ikawa kwamba baba ya Publio alikuwa amelala akitaabishwa na homa na ugonjwa wa kuhara damu, na Paulo akaingia alimokuwa na kusali, akaweka mikono+ yake juu yake akamponya.+ 9 Baada ya jambo hilo kutukia, watu wale wengine kisiwani waliokuwa na magonjwa wakaanza pia kuja kwake na kuponywa.+ 10 Nao pia wakatupa sisi zawadi nyingi na, tulipokuwa tukisafiri, wakapakia vitu kwa ajili ya mahitaji yetu.

11 Miezi mitatu baadaye tukasafiri kutoka Aleksandria+ kwa mashua iliyokuwa imekaa wakati wa majira ya baridi kali katika kisiwa hicho na yenye sanamu ya gubeti ya “Wana wa Zeu.” 12 Nasi tukaegesha katika bandari ya Sirakusa tukakaa siku tatu, 13 mahali ambapo kutoka hapo tulienda tukizunguka na kufika Regiamu. Na siku moja baadaye upepo wa kusini ukazuka nasi tukaingia Puteoli siku ya pili. 14 Tukawakuta akina ndugu hapo nao wakatusihi tukae pamoja nao kwa siku saba; na kwa njia hii tukaja kuelekea Roma. 15 Na kutoka huko akina ndugu, waliposikia habari juu yetu, wakaja kukutana nasi mpaka Soko la Apio na Mikahawa Mitatu na, alipowaona, Paulo akamshukuru Mungu na kujipa moyo.+ 16 Mwishowe, tulipoingia Roma, Paulo akaruhusiwa+ kukaa akiwa peke yake pamoja na askari-jeshi mwenye kumlinda.

17 Hata hivyo, siku tatu baadaye akawaita pamoja wale waliokuwa wakuu wa Wayahudi. Walipokuwa wamekusanyika, akaanza kuwaambia: “Wanaume, akina ndugu, ijapokuwa sikuwa nimefanya jambo lolote kinyume cha watu au desturi za mababu zetu,+ nilitolewa nikiwa mfungwa Yerusalemu na kutiwa mikononi mwa Waroma.+ 18 Na hawa, baada ya kufanya uchunguzi,+ walitaka kunifungua,+ kwa kuwa hakukuwa na sababu yoyote kwangu ya kuuawa.+ 19 Lakini Wayahudi walipoendelea kusema vibaya juu ya jambo hilo, nililazimika kukata rufani+ kwa Kaisari, lakini si kana kwamba nilikuwa na jambo lolote la kushtaki taifa langu. 20 Kwa kweli kwa sababu hii nilisihi niwaone na kusema nanyi, kwa maana nimefungwa mnyororo+ huu kwa sababu ya tumaini+ la Israeli.” 21 Wakamwambia: “Wala sisi hatujapokea barua zinazokuhusu wewe kutoka Yudea, wala hakuna yeyote wa akina ndugu ambaye amefika aliyetujulisha au kusema jambo lolote baya juu yako. 22 Lakini tunaona inafaa kusikia maoni yako kutoka kwako, kwa maana kweli kwa habari ya madhehebu+ hii tunajua kwamba kila mahali huwa inasemwa vibaya.”+

23 Basi wakapanga siku fulani ya kuwa pamoja naye, nao wakaja kwake wakiwa hesabu kubwa zaidi katika makao yake. Naye akawaeleza jambo hilo kwa kutoa ushahidi kamili kuhusiana na ufalme wa Mungu+ na kwa kutumia ushawishi kwao kuhusu Yesu kutoka katika sheria ya Musa+ na pia Manabii,+ tangu asubuhi mpaka jioni. 24 Na wengine wakaanza kuamini+ mambo yaliyosemwa; wengine hawakuamini.+ 25 Kwa hiyo, kwa sababu walikosa kukubaliana, wakaanza kuondoka, huku Paulo akieleza jambo hili moja:

“Roho takatifu kwa kufaa ilisema kupitia Isaya nabii kwa mababu zenu, 26 ikisema, ‘Nenda kwa watu hawa na kusema: “Kwa kusikia, mtasikia lakini msielewe kamwe; na, kutazama, mtatazama, lakini msione kamwe.+ 27 Kwa maana moyo wa watu hawa umekuwa mgumu, na kwa masikio yao wamesikia bila kuitikia, nao wamefunga macho yao; ili wasione kamwe kwa macho yao na kusikia kwa masikio yao na kuelewa kwa moyo wao na kugeuka, nami niwaponye.” ’+ 28 Kwa hiyo jueni kwamba njia hii ambayo Mungu anaitumia kuokoa, imepelekwa nje kwa mataifa;+ wao hakika wataisikiliza.”+ 29 ——

30 Kwa hiyo akakaa miaka miwili kamili katika nyumba yake mwenyewe ya kukodiwa,+ naye akawa akiwakaribisha kwa fadhili wale wote walioingia ndani kwake, 31 akiwahubiria ufalme wa Mungu na kufundisha mambo yanayohusu Bwana Yesu Kristo kwa uhuru wa kusema+ ulio mkubwa zaidi, bila kizuizi.

[Maelezo ya Chini]

Hadesi. Tazama Nyongeza 4.

Hadesi. Tazama Nyongeza 4.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki