Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt Yeremia 1:1-52:34
  • Yeremia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yeremia
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Yeremia

YEREMIA

1 Haya ndiyo maneno ya Yeremia* mwana wa Hilkia, mmoja wa makuhani wa Anathothi+ katika nchi ya Benjamini. 2 Neno la Yehova lilimjia katika siku za Yosia+ mwana wa Amoni,+ mfalme wa Yuda, katika mwaka wa 13 wa utawala wake. 3 Pia lilikuja katika siku za Yehoyakimu+ mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, hadi mwishoni mwa mwaka wa 11 wa utawala wa Sedekia+ mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, mpaka Yerusalemu lilipoenda uhamishoni katika mwezi wa tano.+

4 Neno la Yehova lilinijia, likisema:

 5 “Kabla sijakuumba tumboni nilikujua,*+

Na kabla hujazaliwa* nilikutakasa.*+

Nilikufanya uwe nabii kwa mataifa.”

 6 Lakini nikasema: “Ole wangu, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova!

Mimi sijui kuzungumza,+ kwa maana mimi ni mvulana* tu.”+

 7 Kisha Yehova akaniambia:

“Usiseme, ‘Mimi ni mvulana tu.’

Kwa maana ni lazima uende kwa wote nitakaokutuma kwao,

Nawe unapaswa kusema kila jambo nitakalokuamuru.+

 8 Usiogope kwa sababu ya jinsi wanavyoonekana,+

Kwa maana ‘mimi niko pamoja nawe ili nikuokoe,’+ asema Yehova.”

9 Kisha Yehova akaunyoosha mkono wake na kugusa kinywa changu.+ Na Yehova akaniambia: “Nimeyatia maneno yangu kinywani mwako.+ 10 Tazama, nimekutuma leo hii ili uwe juu ya mataifa na juu ya falme, ili kung’oa na kubomoa, ili kuangamiza na kuangusha, ili kujenga na kupanda.”+

11 Neno la Yehova likanijia tena, likisema: “Unaona nini, Yeremia?” Basi nikasema: “Ninaona tawi la mti wa mlozi.”*

12 Yehova akaniambia: “Uko sahihi, kwa maana niko macho kabisa kuhusu neno langu ili kulitimiza.”

13 Neno la Yehova likanijia mara ya pili, likisema: “Unaona nini?” Basi nikasema: “Ninaona chungu* kinachochemka,* na mdomo wake umeinama kutoka kaskazini.” 14 Kisha Yehova akaniambia:

“Msiba utafunguliwa kutoka kaskazini

Dhidi ya wakaaji wote wa nchi.+

15 Kwa maana ‘ninaziita familia zote za falme za kaskazini,’ asema Yehova,+

‘Nao watakuja; kila mmoja ataweka kiti chake cha ufalme

Kwenye malango ya Yerusalemu,+

Dhidi ya kuta zake pande zote

Na dhidi ya majiji yote ya Yuda.+

16 Nami nitatangaza hukumu zangu dhidi yao kwa sababu ya uovu wao wote,

Kwa sababu wameniacha,+

Nao wanaifukizia miungu mingine moshi wa dhabihu+

Na kuziinamia kazi za mikono yao wenyewe.’+

17 Lakini unapaswa kuwa tayari kuchukua hatua,*

Nawe unapaswa kusimama na kuwaambia kila jambo ninalokuamuru.

Usiwaogope,+

Ili nisikuogopeshe mbele yao.

18 Kwa maana leo nimekufanya uwe jiji lenye ngome,

Nguzo ya chuma, na kuta za shaba dhidi ya nchi yote,+

Kuelekea wafalme wa Yuda na wakuu wake,

Kuelekea makuhani wake na watu wa nchi.+

19 Nao hakika watapigana nawe,

Lakini hawatakushinda,

Kwa maana ‘Mimi niko pamoja nawe,’+ asema Yehova, ‘ili nikuokoe.’”

2 Neno la Yehova likanijia, likisema: 2 “Nenda ukatangaze masikioni mwa watu wa Yerusalemu, ‘Yehova anasema hivi:

“Ninakumbuka vema bidii yako* ulipokuwa kijana,+

Upendo ulioonyesha ulipochumbiwa ili kuolewa,+

Jinsi ulivyonifuata nyikani,

Katika nchi ambayo haipandwi mbegu.+

 3 Israeli alikuwa mtakatifu kwa Yehova,+ mavuno ya kwanza ya mazao yake.”’

‘Yeyote aliyemrarua alikuwa na hatia.

Msiba ulimpata,’ asema Yehova.”+

 4 Sikieni neno la Yehova, enyi watu wa nyumba ya Yakobo,

Nanyi familia zote za nyumba ya Israeli.

 5 Yehova anasema hivi:

“Mababu zenu waliona kosa gani kwangu,+

Hivi kwamba wakatangatanga mbali sana nami,

Wakazifuata sanamu za ubatili,+ nao wenyewe wakawa ubatili?+

 6 Hawakuuliza, ‘Yehova yuko wapi,

Yule aliyetutoa nchini Misri,+

Aliyetuongoza kupitia nyikani,

Kupitia nchi yenye majangwa+ na mashimo,

Kupitia nchi yenye ukame+ na kivuli kizito,

Kupitia nchi ambayo hakuna mtu anayesafiri humo

Na ambamo hakuna mwanadamu anayeishi?’

 7 Kisha nikawaleta ninyi katika nchi yenye mashamba ya matunda,

Ili mle matunda yake na vitu vyake vyema.+

Lakini mliingia humo na kuitia unajisi nchi yangu;

Mkaufanya urithi wangu kuwa kitu kinachochukiza.+

 8 Makuhani hawakuuliza, ‘Yehova yuko wapi?’+

Wale wanaoshughulika na Sheria hawakunijua,

Wachungaji waliniasi,+

Manabii walitabiri kupitia Baali,+

Nao wakawafuata wale ambao hawangewafaidi hata kidogo.

 9 ‘Basi nitapambana zaidi nanyi,’+ asema Yehova,

‘Nami nitapambana na wana wa wana wenu.’

10 ‘Lakini vukeni mpaka nchi za pwani za* Kitimu+ mwone.

Naam, tumeni watu Kedari+ nanyi mfikirie kwa uangalifu;

Mwone ikiwa jambo kama hili limewahi kutendeka.

11 Je, taifa limewahi kubadili miungu yake kwa ajili ya miungu ambayo si miungu?

Lakini watu wangu mwenyewe wamebadili utukufu wangu kwa ajili ya kitu kisicho na maana.+

12 Tazameni jambo hili kwa mshangao, enyi mbingu;

Tetemekeni kwa hofu kubwa,’ asema Yehova,

13 ‘Kwa sababu watu wangu wamefanya mambo mawili mabaya:

Wameniacha mimi, chemchemi ya maji yaliyo hai,+

Na kujichimbia* matangi ya maji,

Matangi yaliyovunjika, ambayo hayawezi kuhifadhi maji.’

14 ‘Je, Israeli ni mtumishi, au ni mtumwa aliyezaliwa nyumbani?

Basi kwa nini amekuwa kitu cha kuporwa?

15 Wanasimba* wananguruma dhidi yake;+

Wameinua sauti zao.

Waliifanya nchi yake kuwa kitu cha kutisha.

Majiji yake yameteketezwa, hivi kwamba hakuna mkaaji.

16 Watu wa Nofu*+ na Tahpanesi+ wanakula utosi wa kichwa chako.

17 Je, hukujiletea jambo hilo

Kwa kumwacha Yehova Mungu wako+

Alipokuwa akikuongoza njiani?

18 Sasa kwa nini unatamani njia ya kwenda Misri+

Ili kunywa maji ya Shihori?*

Kwa nini unatamani njia ya kwenda Ashuru+

Ili kunywa maji ya ule Mto?*

19 Uovu wako unapaswa kukurekebisha,

Na ukosefu wako wa uaminifu unapaswa kukukaripia.

Jua na utambue ubaya na uchungu+ wa

Kumwacha Yehova Mungu wako;

Hujaniogopa,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova wa majeshi.

20 ‘Kwa maana zamani niliivunja nira yako+

Na kuzikata pingu zako.

Lakini ulisema: “Mimi sitatumikia,”

Kwa maana juu ya kila kilima kirefu na chini ya kila mti wenye majani mengi+

Ulilala ukiwa umejinyoosha, ukifanya ukahaba.+

21 Nilikupanda kama mzabibu bora mwekundu,+ wote ukiwa mbegu safi;

Basi umebadilikaje na kuwa machipukizi yaliyoharibika ya mzabibu wa kigeni mbele zangu?’+

22 ‘Hata ukioga kwa magadi na kutumia sabuni nyingi,

Bado hatia yako itakuwa doa mbele zangu,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.

23 Unawezaje kusema, ‘Sijajichafua.

Sijafuata Mabaali?

Angalia njia yako bondeni.

Fikiria ulichofanya.

Wewe ni kama ngamia jike mchanga anayekimbia kasi,

Anayekimbia huku na huku bila mwelekeo katika njia zake,

24 Punda wa mwituni aliyezoea nyika,

Anayenusa upepo katika tamaa yake.*

Ni nani anayeweza kumzuia anaposhikwa na nyege?

Hakuna yeyote kati ya wale wanaomtafuta atakayelazimika kujichosha.

Watampata katika majira yake.*

25 Izuie miguu yako isitembee bila viatu

Na koo lako lisiwe na kiu.

Lakini ulisema, ‘Hakuna tumaini lolote!+

Hakuna! Nimewapenda wageni,*+

Nami nitawafuata.’+

26 Kama aibu ya mwizi anapokamatwa,

Ndivyo watu wa nyumba ya Israeli walivyoaibishwa,

Wao, wafalme wao na wakuu wao,

Makuhani wao na manabii wao.+

27 Wanauambia mti, ‘Wewe ni baba yangu,’+

Na jiwe, ‘Wewe ulinizaa.’

Lakini wamenigeuzia mimi mgongo wao badala ya uso wao.+

Watakapopatwa na msiba watasema,

‘Simama utuokoe!’+

28 Sasa iko wapi miungu yako uliyojitengenezea?+

Na isimame ikiwa inaweza kukuokoa unapopatwa na msiba.

Kwa maana miungu yako imekuwa mingi kama majiji yako, Ee Yuda.+

29 ‘Kwa nini unaendelea kushindana nami?

Kwa nini nyote mmeniasi?’+ asema Yehova.

30 Nimewapiga wana wenu bila matokeo.+

Hawakukubali nidhamu yoyote;+

Upanga wenu wenyewe uliwaangamiza manabii wenu,+

Kama simba anayeshambulia.

31 Enyi kizazi hiki, fikirieni wenyewe neno la Yehova.

Je, nimekuwa kama nyika kwa Israeli

Au nchi yenye giza linalokandamiza?

Kwa nini watu hawa, watu wangu, wamesema, ‘Tunazurura kwa uhuru.

Hatutakuja kwako tena’?+

32 Je, bikira anaweza kuyasahau mapambo yake,

Na bibi harusi mavazi yake ya kifuani?*

Lakini watu wangu wamenisahau mimi kwa siku zisizohesabika.+

33 Ewe mwanamke, jinsi unavyotayarisha njia yako kwa ustadi ili kutafuta upendo!

Umejizoeza katika njia za uovu.+

34 Hata pindo za nguo zako zina madoa ya damu ya maskini* wasio na hatia,+

Ingawa sikuwapata wakivunja ili kuingia;

Imejaa kwenye pindo zako zote.+

35 Lakini unasema, ‘Sina hatia.

Hakika hasira yake imeniondokea.’

Sasa ninaleta hukumu dhidi yako

Kwa sababu unasema, ‘Sijatenda dhambi.’

36 Kwa nini unaiona njia yako isiyo thabiti kuwa jambo dogo?

Utaona aibu kwa sababu ya Misri pia,+

Kama vile ulivyoona aibu kwa sababu ya Ashuru.+

37 Kwa sababu hiyo pia utatoka mikono yako ikiwa juu ya kichwa chako,+

Kwa maana Yehova amewakataa wale unaowategemea;

Hawatakuletea mafanikio.”

3 Watu huuliza: “Mtu akimfukuza mke wake naye aondoke na kuchukuliwa na mwanamume mwingine, je, mtu huyo anapaswa kumrudia tena?”

Je, nchi hiyo haijachafuliwa kabisa?+

“Umefanya ukahaba na marafiki wengi,+

Na je, sasa unapaswa kurudi kwangu?” asema Yehova.

 2 “Inua macho yako kuelekea vilima vitupu uone.

Ni wapi ambapo hukubakwa?

Ulikaa kando ya barabara kwa ajili yao,

Kama mtu anayehamahama* nyikani.

Unaendelea kuichafua nchi

Kwa ukahaba wako na uovu wako.+

 3 Kwa hiyo manyunyu ya mvua yamezuiwa,+

Na hakuna mvua ya masika.

Una uso wenye* ushupavu kama mwanamke anayefanya ukahaba;

Umekataa kuona aibu.+

 4 Lakini sasa unaniambia kwa sauti kubwa,

‘Baba yangu, wewe ni rafiki yangu tangu ujana wangu!+

 5 Je, mtu anapaswa kuendelea kuwa na uchungu milele,

Au kuwa na kinyongo sikuzote?’

Unasema hivyo,

Lakini unaendelea kufanya mambo yote maovu unayoweza kufanya.”+

6 Katika siku za mfalme Yosia,+ Yehova aliniambia: “‘Je, umeona mambo ambayo Israeli asiye mwaminifu ametenda? Amepanda juu ya kila mlima mrefu na kwenda chini ya kila mti wenye majani mengi ili afanye ukahaba.+ 7 Hata baada ya kufanya mambo hayo yote, niliendelea kumwambia arudi kwangu,+ lakini hakurudi; na Yuda akaendelea kumtazama dada yake mwenye hila.+ 8 Nilipoona hivyo, nikamfukuza Israeli asiye mwaminifu akiwa na cheti kamili cha talaka+ kwa sababu ya uzinzi wake.+ Lakini Yuda dada yake mwenye hila hakuogopa; yeye pia alienda na kufanya ukahaba.+ 9 Aliona ukahaba wake kuwa jambo dogo, naye akaendelea kuichafua nchi na kufanya uzinzi na mawe na miti.+ 10 Licha ya hayo yote, Yuda dada yake mwenye hila hakurudi kwangu kwa moyo wake wote, bali kwa kujifanya tu,’ asema Yehova.”

11 Kisha Yehova akaniambia: “Israeli asiye mwaminifu amekuwa mwadilifu kuliko Yuda mwenye hila.+ 12 Nenda uitangazie kaskazini maneno haya:+

“‘“Rudi, Ee Israeli mwasi,” asema Yehova.’+ ‘“Sitakutazama kwa hasira,*+ kwa maana mimi ni mshikamanifu,” asema Yehova.’ ‘“Sitaendelea kuwa na kinyongo milele. 13 Ila tu ukubali hatia yako, kwa maana umemwasi Yehova Mungu wako. Uliendelea kutawanya wema wako* kwa wageni* chini ya kila mti wenye majani mengi, lakini hukuitii sauti yangu,” asema Yehova.’”

14 “Rudini, enyi wana waasi,” asema Yehova. “Kwa maana nimekuwa bwana wenu* wa kweli; nami nitawachukua, mmoja kutoka katika jiji moja na wawili kutoka katika familia moja, nami nitawaleta Sayuni.+ 15 Nami nitawapa wachungaji wanaoupendeza moyo wangu,+ nao watawalisha kwa ujuzi na ufahamu. 16 Mtakuwa wengi nanyi mtazaa matunda nchini siku hizo,” asema Yehova.+ “Hawatasema tena, ‘Sanduku la agano la Yehova!’ Halitaingia moyoni, wala hawatalikumbuka au kulitamani, nalo halitatengenezwa tena. 17 Wakati huo wataliita Yerusalemu kiti cha ufalme cha Yehova;+ na mataifa yote yatakusanywa pamoja kwa jina la Yehova katika Yerusalemu,+ nao hawataufuata tena kwa ukaidi moyo wao mwovu.”

18 “Siku hizo watatembea pamoja, nyumba ya Yuda kando ya nyumba ya Israeli,+ na pamoja watatoka katika nchi ya kaskazini na kuingia katika nchi niliyowapa mababu zenu kuwa urithi.+ 19 Nami nilifikiri, ‘Jinsi nilivyokuweka kati ya wana na kukupa nchi inayotamanika, urithi maridadi zaidi kati ya mataifa!’*+ Pia nilifikiri mtaniita ‘Baba yangu!’ na kwamba hamtageuka na kuacha kunifuata.’ 20 ‘Kwa kweli kama mke anavyomwacha mume wake* kwa hila, ninyi pia, enyi watu wa nyumba ya Israeli, mmenitendea kwa hila,’+ asema Yehova.”

21 Sauti imesikika kwenye vilima vilivyo vitupu,

Kulia na kusihi kwa watu wa Israeli,

Kwa maana wameipotosha njia yao;

Wamemsahau Yehova Mungu wao.+

22 “Rudini, ninyi wana waasi.

Nitaiponya hali yenu ya uasi.”+

“Tupo hapa! Tumekuja kwako,

Kwa maana wewe, Ee Yehova, ni Mungu wetu.+

23 Kwa kweli vilima na machafuko juu ya milima ni udanganyifu.+

Kwa kweli wokovu wa Israeli uko kwa Yehova Mungu wetu.+

24 Lakini jambo la aibu limekula* kazi ngumu ya mababu zetu tangu ujana wetu,+

Makundi yao na mifugo yao,

Wana wao na mabinti wao.

25 Na tulale chini katika aibu yetu,

Fedheha yetu na itufunike,

Kwa maana tumemtendea dhambi Yehova Mungu wetu,+

Sisi na baba zetu tangu ujana wetu mpaka leo hii,+

Nasi hatujaitii sauti ya Yehova Mungu wetu.”

4 “Ukirudi, Ee Israeli,” asema Yehova,

“Ukirudi kwangu

Na ukiondoa sanamu zako zenye kuchukiza kutoka mbele zangu,

Basi hutakuwa mkimbizi.+

 2 Nawe ukiapa,

‘Kwa hakika kama Yehova anavyoishi!’ katika kweli, haki, na uadilifu,

Ndipo mataifa yatakapojipatia baraka kupitia yeye,

Nayo yatajigamba kwa sababu yake.”+

3 Kwa maana Yehova anawaambia hivi watu wa Yuda na Yerusalemu:

“Jilimieni shamba linalofaa kwa kilimo,

Nanyi msiendelee kupanda kati ya miiba.+

 4 Jitahirini kwa ajili ya Yehova,

Na kuondoa magovi ya mioyo yenu,+

Ninyi watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu,

Ili ghadhabu yangu isiwake kama moto

Na iteketeze bila yeyote wa kuizima,

Kwa sababu ya matendo yenu maovu.”+

 5 Tangazeni jambo hilo Yuda, na kulihubiri Yerusalemu.

Pazeni sauti na kupiga pembe katika nchi yote.+

Iteni kwa sauti na kusema: “Kusanyikeni pamoja,

Nasi tukimbilie katika majiji yenye ngome.+

 6 Inueni ishara* kuelekea Sayuni.

Tafuteni kimbilio, na msisimame tuli,”

Kwa maana ninaleta msiba kutoka kaskazini,+ kishindo kikubwa.

 7 Ametokea kama simba kutoka kwenye kichaka chake;+

Yule anayeyaangamiza mataifa ametoka.+

Ametoka mahali pake ili kuifanya nchi yako kuwa kitu cha kutisha.

Majiji yako yatakuwa magofu, bila mkaaji.+

 8 Kwa hiyo, vaeni nguo za magunia,+

Ombolezeni* na kupiga mayowe,

Kwa sababu hasira ya Yehova inayowaka haijaondoka juu yetu.

 9 “Siku hiyo,” asema Yehova, “mfalme atakufa moyo,*+

Pia wakuu watakufa moyo;*

Makuhani watashikwa na hofu, nao manabii watashangaa.”+

10 Kisha nikasema: “Ole wangu, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Kwa kweli umewadanganya kabisa watu hawa+ na Yerusalemu, kwa kusema, ‘Mtakuwa na amani,’+ wakati upanga uko kwenye koo zetu.”*

11 Wakati huo watu hawa na Yerusalemu wataambiwa:

“Upepo unaokausha kutoka kwenye vilima vitupu vya jangwani

Utavuma juu ya binti ya* watu wangu;

Hauji kupepeta wala kusafisha.

12 Upepo unaovuma kwa nguvu zote unatoka sehemu hizo kwa amri yangu.

Sasa nitatangaza hukumu dhidi yao.

13 Tazameni! Atakuja kama mawingu ya mvua,

Na magari yake ni kama upepo wa dhoruba.+

Farasi wake wanakimbia kwa kasi kuliko tai.+

Ole wetu, kwa sababu tumeangamia!

14 Usafishe moyo wako uwe safi kutokana na uovu, Ee Yerusalemu, ili uokolewe.+

Utafikiria mambo maovu mpaka lini?

15 Kwa maana sauti inaleta habari kutoka Dani,+

Nayo inatangaza msiba kutoka kwenye milima ya Efraimu.

16 Tangazeni jambo hilo, naam, kwa mataifa;

Litangazeni dhidi ya Yerusalemu.”

“Walinzi* wanakuja kutoka nchi ya mbali,

Nao watapaza sauti zao dhidi ya majiji ya Yuda.

17 Wanamshambulia kutoka pande zote kama walinzi wa shamba ambalo halijazingirwa na ukuta,+

Kwa sababu ameniasi,”+ asema Yehova.

18 “Njia zako mwenyewe na matendo yako yataletwa juu yako.+

Jinsi msiba wako ulivyo mchungu,

Kwa maana umefika mpaka moyoni mwako!”

19 Jamani maumivu yangu,* maumivu yangu!

Ninahisi uchungu mwingi moyoni mwangu.*

Moyo wangu unapigapiga ndani yangu.

Siwezi kunyamaza,

Kwa maana nimesikia* sauti ya pembe,

King’ora cha vita.*+

20 Msiba baada ya msiba umetangazwa,

Kwa maana nchi yote imeharibiwa.

Kwa ghafla, mahema yangu mwenyewe yameharibiwa,

Kwa muda mfupi, vitambaa vya mahema yangu.+

21 Nitaendelea kuona ishara* mpaka lini,

Na kuendelea kusikia sauti ya pembe?+

22 Kwa maana watu wangu ni wajinga;+

Hawanitambui.

Wao ni wana wapumbavu, wasio na uelewaji.

Ni werevu* sana katika kutenda maovu,

Lakini hawajui kutenda mema.

23 Niliiona nchi, na tazama! ilikuwa tupu na ukiwa.+

Nilitazama mbingu, na nuru yake haikuwepo.+

24 Niliiona milima, na tazama! ilikuwa ikitetemeka,

Na vilima vilikuwa vikitikisika.+

25 Niliona, na tazama! hapakuwa na mtu yeyote,

Na ndege wote wa angani walikuwa wamekimbia.+

26 Niliona, na tazama! sasa shamba la matunda lilikuwa nyika,

Na majiji yake yote yalikuwa yamebomolewa.+

Ilikuwa kwa sababu ya Yehova,

Kwa sababu ya hasira yake inayowaka.

27 Kwa maana Yehova anasema hivi: “Nchi yote itaachwa ukiwa,+

Lakini sitaiangamiza kabisa.

28 Kwa sababu hiyo nchi itaomboleza,+

Na juu mbingu zitakuwa na giza.+

Ni kwa sababu nimesema, nami nimeamua,

Nami sitabadili nia yangu,* wala sitaliacha jambo hilo.+

29 Kwa sababu ya sauti ya wapanda farasi na wapiga-mishale,

Jiji zima linakimbia.+

Wanaingia vichakani,

Nao wanapanda kwenye miamba.+

Kila jiji linaachwa,

Na hakuna mtu anayeishi humo.”

30 Sasa kwa kuwa umeangamizwa, utafanya nini?

Ulikuwa ukivaa nguo nyekundu,

Ukijipamba kwa mapambo ya dhahabu,

Na kupanua macho yako kwa kuyapaka rangi nyeusi.*

Lakini ulijirembesha bure,+

Kwa maana waliokutamani wamekukataa;

Sasa wanataka kukuua.+

31 Kwa maana nimesikia sauti kama ya mwanamke mgonjwa,

Maumivu kama ya mwanamke anayezaa mtoto wake wa kwanza,

Sauti ya binti ya Sayuni ambaye anaendelea kuhemahema kwa nguvu.

Anasema hivi akiinyoosha mikono yake:+

“Ole wangu, kwa maana nimechoka* kwa sababu ya wauaji!”

5 Tembeeni huku na huku katika barabara za Yerusalemu.

Tazameni pande zote mwone.

Tafuteni katika viwanja vyake vya jiji

Ikiwa mnaweza kumpata mtu anayetenda haki,+

Yeyote anayejitahidi kuwa mwaminifu,

Nami nitalisamehe jiji hilo.

 2 Hata wakisema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi!”

Bado wataapa kwa uwongo.+

 3 Ee Yehova, je, macho yako hayatafuti uaminifu?+

Uliwapiga, lakini hawakusikia.*

Uliwaangamiza, lakini walikataa kukubali nidhamu.+

Walizifanya nyuso zao kuwa ngumu kuliko mwamba,+

Nao wakakataa kugeuka.+

 4 Lakini nilisema moyoni: “Kwa hakika hawa ni watu wa hali ya chini.

Wanatenda kwa upumbavu, kwa sababu hawaijui njia ya Yehova,

Hukumu ya Mungu wao.

 5 Nitaenda kwa watu mashuhuri na kuzungumza nao,

Kwa maana lazima wameijua njia ya Yehova,

Hukumu ya Mungu wao.+

Lakini wote walikuwa wameivunja nira

Na kuvikata vizuizi.”*

 6 Ndiyo sababu simba kutoka msituni anawashambulia,

Mbwamwitu wa majangwa tambarare anaendelea kuwararua,

Chui anakaa macho kwenye majiji yao.

Kila mtu anayetoka humo anararuliwa vipandevipande.

Kwa maana makosa yao ni mengi;

Matendo yao ya ukosefu wa uaminifu ni mengi sana.+

 7 Ninawezaje kukusamehe kwa jambo hili?

Wana wako wameniacha,

Nao wanaapa kwa kitu ambacho si Mungu.+

Nilitosheleza mahitaji yao,

Lakini waliendelea kufanya uzinzi,

Na kukusanyika katika nyumba ya kahaba.

 8 Wao ni kama farasi wenye tamaa na uchu,

Kila mmoja anamlilia mke wa mwenzake.+

 9 “Je, sipaswi kuwafanya wawajibike kwa sababu ya mambo haya?” asema Yehova.

“Je, sipaswi* kujilipizia kisasi dhidi ya taifa kama hili?”+

10 “Pandeni mshambulie matuta yake ya mizabibu na kuyaharibu,

Lakini msiyaharibu kabisa.+

Ondoeni machipukizi yake yanayoenea,

Kwa maana si ya Yehova.

11 Kwa sababu watu wa nyumba ya Israeli na watu wa nyumba ya Yuda

Wamenitendea kwa hila kabisa,” asema Yehova.+

12 “Wamemkana Yehova, nao wanaendelea kusema,

‘Hatafanya chochote.*+

Hatutapatwa na msiba wowote;

Hatutaona upanga wala njaa kali.’+

13 Manabii wamejaa upepo,

Na neno* halimo ndani yao.

Na iwe hivyo kwao!”

14 Kwa hiyo, Yehova, Mungu wa majeshi, anasema hivi:

“Kwa sababu watu hawa wanasema jambo hilo,

Ninayafanya maneno yangu kuwa moto kinywani mwako,+

Na watu hawa ndio kuni,

Nao utawateketeza.”+

15 “Tazameni, ninaleta dhidi yenu taifa kutoka mbali, Enyi watu wa nyumba ya Israeli,”+ asema Yehova.

“Ni taifa linalodumu.

Ni taifa la zamani za kale,

Taifa ambalo lugha yake hamwijui,

Na hamwezi kuelewa wanachosema.+

16 Podo lao ni kama kaburi lililo wazi;

Wote ni mashujaa.

17 Watakula mavuno yenu na mkate wenu.+

Watawala wana wenu na mabinti wenu.

Watayala makundi yenu na mifugo yenu.

Wataila mizabibu yenu na mitini yenu.

Watayaangamiza kwa upanga majiji yenu yenye ngome mnayoyatumaini.”

18 “Lakini hata katika siku hizo,” asema Yehova, “sitawaangamiza kabisa.+ 19 Na wakiuliza, ‘Kwa nini Yehova Mungu wetu ametutendea mambo haya yote?’ mtawajibu, ‘Kama mlivyoniacha ili kumtumikia mungu wa kigeni katika nchi yenu, ndivyo mtakavyowatumikia wageni katika nchi isiyo yenu.’”+

20 Tangazeni jambo hili katika nyumba ya Yakobo,

Na kulitangaza Yuda, mkisema:

21 “Sikieni jambo hili, ninyi watu wajinga na wasio na akili:*+

Wana macho lakini hawawezi kuona;+

Wana masikio lakini hawawezi kusikia.+

22 ‘Je, hamniogopi mimi?’ asema Yehova,

‘Je, hampaswi kutetemeka mbele zangu?

Mimi ndiye niliyeweka mchanga kuwa mpaka wa bahari,

Sheria inayodumu isiyoweza kukiukwa na bahari.

Ingawa mawimbi yake yanasukasuka, hayawezi kushinda;

Ingawa yananguruma, bado hayawezi kuvuka.+

23 Lakini watu hawa wana moyo mgumu unaoasi;

Wamegeuka kando na kuifuata njia yao wenyewe.+

24 Nao hawasemi moyoni mwao:

“Sasa na tumwogope Yehova Mungu wetu,

Yule anayeleta mvua katika majira yake,

Mvua ya vuli na mvua ya masika,

Yule anayetulindia majuma yaliyowekwa ya mavuno.”+

25 Makosa yenu wenyewe yalizuia mambo haya yasije;

Dhambi zenu wenyewe zimewanyima mambo mema.+

26 Kwa maana kati ya watu wangu kuna watu waovu.

Wanaendelea kuchungulia, kama wawindaji wa ndege wanapochutama.

Wanatega mtego hatari.

Wanawanasa watu.

27 Kama kizimba kilichojaa ndege,

Ndivyo nyumba zao zilivyojaa udanganyifu.+

Ndiyo sababu wamekuwa wenye nguvu na matajiri.

28 Wamenenepa na kuwa laini;

Wanafurika uovu.

Hawawatetei mayatima katika kesi,+

Wanatafuta mafanikio yao wenyewe;

Nao wanawanyima haki maskini.’”+

29 “Je, sipaswi kuwafanya wawajibike kwa sababu ya mambo haya,” asema Yehova.

“Je, sipaswi* kujilipizia kisasi dhidi ya taifa kama hili?

30 Jambo la kutisha na kuchukiza limetokea nchini:

31 Manabii wanatabiri uwongo,+

Nao makuhani wanakandamiza kwa mamlaka yao wenyewe.

Na watu wangu wanapenda mambo yawe hivyo.+

Lakini mtafanya nini mwisho ukifika?”

6 Kimbilieni usalama, enyi wana wa Benjamini, mbali na Yerusalemu.

Pigeni pembe+ huko Tekoa;+

Washeni ishara ya moto Beth-hakeremu!

Kwa maana msiba unakuja kutoka kaskazini, msiba mkubwa.+

 2 Binti ya Sayuni anafanana na mwanamke mrembo na mwororo.+

 3 Wachungaji watakuja na mifugo yao.

Watapiga mahema yao kumzunguka pande zote,+

Kila mmoja akilisha mifugo anayotunza.+

 4 “Jitayarisheni kupigana vita naye!*

Simameni, tumshambulie wakati wa adhuhuri!”

“Ole wetu, kwa maana siku inakwisha,

Kwa maana vivuli vya jioni vinarefuka!”

 5 “Simameni, tumshambulie usiku

Na kuiharibu minara yake yenye ngome.”+

 6 Kwa maana Yehova wa majeshi anasema hivi:

“Kateni miti na mjenge boma la kuzingira Yerusalemu.+

Yeye ni jiji ambalo lazima liadhibiwe;*

Hamna lolote ndani yake isipokuwa ukandamizaji.+

 7 Kama tangi linavyohifadhi maji yake yakiwa baridi,

Ndivyo anavyohifadhi uovu wake ukiwa baridi.

Ukatili na maangamizi yanasikiwa ndani yake;+

Ugonjwa na tauni viko mbele zangu daima.

 8 Nakuonya, Ee Yerusalemu, la sivyo nitakuacha* kwa chuki;+

Nitakufanya uwe ukiwa, nchi isiyo na wakaaji.”+

 9 Yehova wa majeshi anasema hivi:

“Watawaokota kikamilifu Waisraeli watakaobaki kama zabibu za mwisho zilizo kwenye mzabibu.

Pitisha mkono wako tena kama mtu anayekusanya zabibu kwenye mizabibu.”

10 “Nitazungumza na nani na kumwonya?

Ni nani atakayesikiliza?

Tazama! Masikio yao yamezibwa* hivi kwamba hawawezi kusikiliza.+

Tazama! Neno la Yehova limekuwa kitu wanachokidharau;+

Hawapendezwi nalo.

11 Basi nimejawa na ghadhabu ya Yehova,

Nami nimechoka kuizuia ndani yangu.”+

“Imwage juu ya mtoto aliye barabarani,+

Juu ya vikundi vya vijana waliokusanyika pamoja.

Wote watakamatwa, mwanamume pamoja na mke wake,

Wazee pamoja na waliozeeka sana.*+

12 Watu wengine watapewa nyumba zao,

Pamoja na mashamba yao na wake zao.+

Kwa maana nitaunyoosha mkono wangu dhidi ya wakaaji wa nchi,” asema Yehova.

13 “Kwa maana kuanzia mdogo zaidi mpaka mkubwa zaidi, kila mmoja anajipatia faida isiyo ya haki;+

Kuanzia nabii mpaka kuhani, kila mmoja anatenda kwa ulaghai.+

14 Nao wanajaribu kuponya kijuujuu jeraha* la watu wangu, wakisema,

‘Kuna amani! Kuna amani!’

Wakati hakuna amani.+

15 Je, wanaona aibu kwa sababu ya mambo yanayochukiza waliyotenda?

Hawaoni aibu hata kidogo!

Hata hawajui jinsi ya kufedheheka!+

Basi wataanguka miongoni mwa wale walioanguka.

Nitakapowaadhibu watajikwaa,” asema Yehova.

16 Yehova anasema hivi:

“Simameni kwenye makutano ya barabara mwone.

Ulizeni kuhusu barabara za zamani za kale,

Ulizeni mahali ilipo njia nzuri, nanyi mtembee ndani yake,+

Nanyi mtajipumzisha.”*

Lakini wanasema: “Hatutatembea kwenye njia hiyo.”+

17 “Nami nikawaweka walinzi+ waliosema,

‘Isikilizeni sauti ya pembe!’”+

Lakini wakasema: “Hatutaisikiliza.”+

18 “Kwa hiyo sikieni, enyi mataifa!

Nawe ujue, Ee kusanyiko,

Jambo litakalowapata.

19 Sikiliza, Ee dunia!

Ninawaletea msiba watu hawa+

Kama matunda ya mipango yao,

Kwa maana hawakuyasikiliza maneno yangu

Nao waliikataa sheria* yangu.”

20 “Ninafaidikaje mnapoleta ubani kutoka Sheba

Na utete wenye manukato kutoka nchi ya mbali?

Dhabihu zenu nzima za kuteketezwa hazikubaliki,

Na dhabihu zenu hazinipendezi.”+

21 Kwa hiyo Yehova anasema hivi:

“Ninawawekea watu hawa vikwazo,

Nao watajikwaa juu yake,

Akina baba na wana pia,

Jirani na mwenzake,

Nao wataangamia wote.”+

22 Yehova anasema hivi:

“Tazama! Watu wanakuja kutoka nchi ya kaskazini,

Na taifa kubwa litaamshwa kutoka sehemu za mbali zaidi za dunia.+

23 Watashika upinde na mkuki.

Ni wakatili na hawatakuwa na huruma.

Sauti yao itanguruma kama bahari,

Nao wanapanda farasi.+

Wanajipanga kivita dhidi yako kama mwanamume wa vita, Ee binti ya Sayuni.”

24 Tumesikia habari zake.

Mikono yetu imelegea.+

Taabu imetushika,

Maumivu kama ya* mwanamke anayezaa.+

25 Usiende shambani,

Wala usitembee barabarani,

Kwa maana adui ana upanga;

Kuna hofu kila upande.

26 Ee binti ya watu wangu,

Vaa nguo za magunia+ na ugaegae katika majivu.

Omboleza kana kwamba unamwombolezea mwana wa pekee, kwa kilio cha uchungu,+

Kwa maana mwangamizaji atatushambulia kwa ghafla.+

27 “Nimekufanya wewe* kuwa mpimaji wa madini miongoni mwa watu wangu,

Mtu anayefanya uchunguzi kamili;

Unapaswa kuangalia na kuchunguza njia yao.

28 Wote ni watu wakaidi kabisa,+

Wanaotembea huku na huku wakichongea.+

Wao ni kama shaba na chuma;

Wote wamepotoka.

29 Vifaa vya kuvukuta vimeunguzwa.

Risasi inatoka kwenye moto wao.

Mtu anaendelea kuwasafisha sana lakini anafanya kazi ya bure,+

Na wale wabaya hawajatengwa.+

30 Hakika watu watawaita fedha iliyokataliwa,

Kwa maana Yehova amewakataa.”+

7 Hili ndilo neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Yehova, likisema: 2 “Simama katika lango la nyumba ya Yehova nawe utangaze hapo ujumbe huu, ‘Sikieni neno la Yehova ninyi watu wote wa Yuda mnaoingia katika malango haya ili kumwinamia Yehova. 3 Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Rekebisheni njia zenu na matendo yenu, nami nitawaruhusu mwendelee kukaa mahali hapa.+ 4 Msiyatumaini maneno ya udanganyifu na kusema, ‘Hili ni* hekalu la Yehova, hekalu la Yehova, hekalu la Yehova!’+ 5 Mkirekebisha kikweli njia zenu na matendo yenu; mkitekeleza haki kikweli kati ya mtu na jirani yake;+ 6 msipowakandamiza wakaaji wageni, mayatima,* na wajane;+ msipomwaga damu isiyo na hatia mahali hapa; na msipoifuata miungu mingine na kujiletea madhara;+ 7 basi nitawaruhusu mwendelee kukaa mahali hapa, katika nchi niliyowapa mababu zenu daima.”’”*

8 “Lakini mnayatumaini maneno ya udanganyifu+—hayatawaletea faida yoyote. 9 Je, mnaweza kuiba,+ kuua, kufanya uzinzi, kuapa kwa uwongo,+ kumtolea dhabihu* Baali,+ na kuifuata miungu mingine ambayo hamkuijua, 10 kisha mje na kusimama mbele zangu katika nyumba hii inayoitwa kwa jina langu na kusema, ‘Tutaokolewa,’ ilhali mnafanya mambo hayo yote yanayochukiza? 11 Je, nyumba hii inayoitwa kwa jina langu imekuwa pango la wanyang’anyi machoni penu?+ Nimejionea jambo hilo,” asema Yehova.

12 “‘Hata hivyo, sasa nendeni mahali pangu huko Shilo,+ ambapo mwanzoni nilifanya jina langu likae,+ na kuona nilivyopafanya kwa sababu ya uovu wa watu wangu Waisraeli.+ 13 Lakini mliendelea kufanya mambo hayo yote,’ asema Yehova, ‘na ingawa nilizungumza nanyi tena na tena,* hamkusikiliza.+ Niliendelea kuwaita, lakini hamkujibu.+ 14 Ndivyo nitakavyoitendea nyumba inayoitwa kwa jina langu,+ ambayo mnaitumaini,+ na mahali hapa ambapo niliwapa ninyi na mababu zenu, kama nilivyoitendea Shilo.+ 15 Nitawatupa kutoka mbele za macho yangu, kama nilivyowatupa ndugu zenu wote, wazao wote wa Efraimu.’+

16 “Lakini wewe, usisali kwa ajili ya watu hawa. Usipaze kilio wala kusali wala kunisihi kwa ajili yao,+ kwa maana sitakusikiliza.+ 17 Je, huoni mambo wanayofanya katika majiji ya Yuda na kwenye barabara za Yerusalemu? 18 Wana wanakusanya kuni, akina baba wanawasha moto, na wake wanakanda unga ili kumwokea Malkia wa Mbinguni*+ keki za dhabihu, nao wanaimiminia miungu mingine matoleo ya kinywaji ili wanikasirishe.+ 19 ‘Lakini je, ni mimi wanayeniumiza?’* auliza Yehova. ‘Je, hawajiumizi wao wenyewe, kwa aibu yao wenyewe?’+ 20 Kwa hiyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema, ‘Tazama! Hasira yangu na ghadhabu yangu zitamwagwa mahali hapa,+ juu ya mwanadamu na mnyama, juu ya miti ya shambani na mazao ya ardhi; itateketeza na haitazimwa.’+

21 “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema, ‘Endeleeni, ongezeni dhabihu zenu nzima za kuteketezwa kwenye dhabihu zenu nyingine, na mle nyama hizo ninyi wenyewe.+ 22 Kwa maana siku niliyowatoa mababu zenu nchini Misri, sikuwaambia wala kuwaamuru kuhusu dhabihu nzima za kuteketezwa na dhabihu nyingine.+ 23 Lakini niliwaamuru hivi: “Tiini sauti yangu, nami nitakuwa Mungu wenu, nanyi mtakuwa watu wangu.+ Ni lazima mtembee katika njia yote ninayowaamuru, ili mambo yawaendee vema.”’+ 24 Lakini hawakusikiliza wala kutega sikio lao;+ badala yake walitembea katika mipango yao* wenyewe, wakifuata kwa ukaidi moyo wao mwovu,+ nao wakarudi nyuma, badala ya kwenda mbele, 25 tangu siku ambayo mababu zenu walitoka nchini Misri mpaka leo hii.+ Basi nikaendelea kuwatuma kwenu watumishi wangu wote manabii, nilikuwa nikiwatuma kila siku, tena na tena.*+ 26 Lakini walikataa kunisikiliza, nao hawakutega sikio lao.+ Badala yake, walikuwa wakaidi,* nao walitenda mambo mabaya zaidi kuliko mababu zao!

27 “Utawaambia maneno haya yote,+ lakini hawatakusikiliza; utawaita, lakini hawatakujibu. 28 Nawe utawaambia, ‘Hili ndilo taifa ambalo halikuitii sauti ya Yehova Mungu wao, nao walikataa kukubali nidhamu. Uaminifu umetoweka na hata hautajwi miongoni mwao.’*+

29 “Nyoa nywele zako ambazo hazijanyolewa,* nawe uzitupe, na uimbe wimbo wa huzuni* juu ya vilima vitupu, kwa maana Yehova amekikataa na atakiacha kizazi hiki ambacho kimemkasirisha. 30 ‘Kwa maana watu wa Yuda wametenda maovu machoni pangu,’ asema Yehova. ‘Wameziweka sanamu zao zinazochukiza katika nyumba ambayo imeitwa kwa jina langu, ili kuitia unajisi.+ 31 Wamejenga mahali pa juu pa Tofethi, palipo katika Bonde la Mwana wa Hinomu,*+ ili kuwateketeza motoni wana wao na mabinti wao,+ jambo ambalo sikuamuru na ambalo hata halijawahi kamwe kuingia moyoni mwangu.’*+

32 “‘Kwa hiyo tazama! siku zinakuja,’ asema Yehova, ‘wakati ambapo bonde hilo halitaitwa tena Tofethi au Bonde la Mwana wa Hinomu* bali Bonde la Mauaji. Watawazika wafu katika Tofethi hivi kwamba hakutakuwa na nafasi zaidi.+ 33 Na maiti za watu hawa zitakuwa chakula cha ndege wa angani na cha wanyama wa duniani, na hakuna mtu atakayewafukuza.+ 34 Nitaikomesha sauti ya furaha na sauti ya shangwe, sauti ya bwana harusi na sauti ya bibi harusi,+ katika majiji ya Yuda na katika barabara za Yerusalemu, kwa maana nchi itakuwa magofu.’”+

8 “Wakati huo,” asema Yehova, “mifupa ya wafalme wa Yuda, mifupa ya wakuu wake, mifupa ya makuhani, mifupa ya manabii, na mifupa ya wakaaji wa Yerusalemu itatolewa katika makaburi yao. 2 Itatandazwa juani na mbele ya mwezi na kwa jeshi lote la mbinguni ambalo wamelipenda na kulitumikia na kulifuata na kulitafuta na kuliinamia.+ Haitakusanywa, wala haitazikwa. Itakuwa kama mbolea juu ya ardhi.”+

3 “Na wale watakaobaki na kuokoka wa familia hii yenye uovu watachagua kifo badala ya uhai katika sehemu zote ambazo nitawatawanya,” asema Yehova wa majeshi.

4 “Nawe unapaswa kuwaambia, ‘Yehova anasema hivi:

“Je, wataanguka na wasisimame tena?

Mtu akigeuka, je, yule mwingine hatageuka pia?

 5 Kwa nini watu hawa, Yerusalemu, wanakosa uaminifu kwa ukosefu wa uaminifu unaodumu?

Wanashika kwa nguvu udanganyifu;

Wanakataa kugeuka.+

 6 Nilitega sikio na kuendelea kusikiliza, lakini mazungumzo yao hayakuwa mazuri.

Hakuna mtu aliyetubu uovu wake au kuuliza, ‘Nimefanya nini?’+

Kila mmoja anarudi tena na tena kwenye njia inayopendwa na wengi, kama farasi anayekimbia kasi kuingia vitani.

 7 Hata korongo angani anajua majira yake;*

Njiwa tetere na mbayuwayu na teleka* hawachelewi kurudi.*

Lakini watu wangu hawaelewi hukumu ya Yehova.”’+

 8 ‘Mnawezaje kusema: “Tuna hekima, nasi tuna sheria* ya Yehova”?

Kwa hakika, kalamu ya uwongo*+ ya waandishi imetumiwa kuandika uwongo tu.

 9 Wenye hekima wameaibishwa.+

Wameogopa nao watashikwa.

Tazama! Wamelikataa neno la Yehova,

Nao wana hekima gani?

10 Basi nitawapa wanaume wengine wake zao,

Na mashamba yao nitawapa wamiliki wengine;+

Kwa maana kuanzia mdogo zaidi mpaka mkubwa zaidi, kila mmoja anajipatia faida isiyo ya haki;+

Kuanzia nabii mpaka kuhani, kila mmoja anatenda kwa ulaghai.+

11 Nao wanajaribu kuponya kijuujuu jeraha* la binti ya watu wangu, wakisema,

“Kuna amani! Kuna amani!”

Wakati hakuna amani.+

12 Je, wanaona aibu kwa sababu ya mambo yenye kuchukiza waliyotenda?

Hawaoni aibu hata kidogo!

Hata hawajui jinsi ya kufedheheka!+

Basi wataanguka kati ya wale walioanguka.

Nitakapowaletea adhabu watajikwaa,”+ asema Yehova.

13 ‘Nitakapowakusanya, nitawamaliza,’ asema Yehova.

‘Hakutakuwa na zabibu zitakazobaki kwenye mzabibu, wala tini kwenye mtini, na majani yatanyauka.

Nao watapoteza kile nilichowapa.’”

14 “Kwa nini tunaketi hapa?

Tukusanyikeni pamoja tuingie katika majiji yenye ngome+ na kuangamia humo.

Kwa maana Yehova Mungu wetu atatuangamiza,

Naye anatupatia maji yenye sumu tunywe,+

Kwa sababu tumemtendea Yehova dhambi.

15 Tulitumaini kupata amani, lakini hakuna jambo lolote jema lililokuja,

Wakati wa kuponywa, lakini kuna hofu!+

16 Mikoromo ya farasi wake inasikika kutoka Dani.

Kwa sababu ya mlio wa farasi dume wake,

Nchi nzima inatetemeka.

Wanaingia na kuinyafua nchi na kila kitu kilichomo,

Jiji na wakaaji wake.”

17 “Kwa maana ninawatuma nyoka kati yenu,

Nyoka wenye sumu wasioweza kuchezeshwa,

Nao hakika watawauma,” asema Yehova.

18 Huzuni yangu haiwezi kuponywa;

Moyo wangu ni mgonjwa.

19 Kutoka nchi ya mbali kuna kilio cha kuomba msaada

Kutoka kwa binti ya watu wangu:

“Je, Yehova hayuko Sayuni?

Au je, mfalme wake hayuko ndani yake?”

“Kwa nini wamenikasirisha kwa sanamu zao za kuchongwa,

Kwa miungu yao ya kigeni ya ubatili?”

20 “Mavuno yamepita, kiangazi kimeisha,

Lakini hatujaokolewa!”

21 Nimevunjwavunjwa kwa sababu ya jeraha* la binti ya watu wangu;+

Nimehuzunika.

Nimepatwa na mshtuko.

22 Je, hakuna zeri* kule Gileadi?+

Au, je, hakuna mponyaji* huko?+

Kwa nini binti ya watu wangu hajaponywa?+

9 Laiti kichwa changu kingekuwa maji,

Na macho yangu chemchemi ya machozi!+

Ndipo ningelia usiku na mchana

Kwa ajili ya watu wangu waliouawa.

 2 Laiti ningepata mahali ambapo wasafiri hulala nyikani!

Ndipo ningewaacha watu wangu na kwenda mbali nao,

Kwa maana wote ni wazinzi,+

Kundi la watu wenye hila.

 3 Wanaupinda ulimi wao kama upinde;

Uwongo, badala ya uaminifu, umeenea nchini.+

“Wanatoka uovu hadi uovu zaidi,

Nao hawanisikilizi,”+ asema Yehova.

 4 “Kila mtu, jihadhari na jirani yako,

Wala usimwamini hata ndugu yako.

Kwa maana kila ndugu ni msaliti,+

Na kila jirani ni mchongezi.+

 5 Kila mtu anamdanganya jirani yake,

Na hakuna yeyote anayesema ukweli.

Wameufundisha ulimi wao kusema uwongo.+

Wanajichosha kwa kufanya makosa.

 6 Unaishi katikati ya udanganyifu.

Katika udanganyifu wao walikataa kunijua mimi,” asema Yehova.

 7 Kwa hiyo Yehova wa majeshi anasema hivi:

“Nitawayeyusha na kuwajaribu,+

Kwa maana ni nini kingine ninachoweza kumtendea binti ya watu wangu?

 8 Ulimi wao ni mshale unaoua na kusema udanganyifu.

Kwa kinywa chake mtu anazungumza na jirani yake kuhusu amani,

Lakini ndani anamvizia.”

 9 “Je, sipaswi kuwafanya wawajibike kwa sababu ya mambo haya?” asema Yehova.

“Je, sipaswi* kujilipizia kisasi dhidi ya taifa kama hili?+

10 Nitalia na kuiombolezea milima

Na kuimba wimbo wa huzuni* kwa ajili ya malisho ya nyikani,

Kwa maana yameteketezwa hivi kwamba hakuna mwanadamu anayepita humo,

Na sauti ya mifugo haisikiwi.

Ndege wa angani na wanyama wamekimbia; wametoweka.+

11 Nitalifanya Yerusalemu kuwa rundo la mawe,+ mapango ya mbwamwitu,+

Nami nitayafanya majiji ya Yuda yawe ukiwa, bila mkaaji.+

12 Ni nani mwenye hekima ya kutosha kuelewa jambo hili?

Kinywa cha Yehova kimezungumza na nani, ili atangaze jambo hilo?

Kwa nini nchi imeangamia?

Kwa nini imeteketezwa kama nyika,

Hivi kwamba hakuna mtu anayepita humo?”

13 Yehova akajibu: “Kwa sababu wameikataa sheria* yangu niliyowapa, na kwa sababu hawajaifuata na kutii sauti yangu. 14 Badala yake, walifuata kwa ukaidi mioyo yao wenyewe,+ na kuzifuata sanamu za Baali, kama baba zao walivyowafundisha kufanya.+ 15 Kwa hiyo, Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Tazama, ninawafanya watu hawa wale pakanga, nami nitawafanya wanywe maji yenye sumu.+ 16 Nitawatawanya kati ya mataifa ambayo wao na baba zao hawajayajua,+ nami nitatuma upanga uwafuate mpaka nitakapowaangamiza kabisa.’+

17 Yehova wa majeshi anasema hivi:

‘Tendeni kwa uelewaji.

Waiteni wanawake wanaoimba nyimbo za huzuni,*+

Nanyi waiteni wanawake stadi waje,

18 Ili waje haraka na kutuombolezea,

Ili macho yetu yabubujike machozi

Na kope zetu zitiririke maji.+

19 Kwa maana sauti ya maombolezo imesikika kutoka Sayuni:+

“Jinsi tulivyoangamizwa!

Jinsi aibu yetu ilivyo nyingi!

Kwa maana tumeiacha nchi, nao wamezibomoa nyumba zetu.”+

20 Enyi wanawake, sikieni neno la Yehova.

Sikio lenu na lipokee neno la kinywa chake.

Wafundisheni mabinti wenu maombolezo haya,

Na mfundishane wimbo huu wa huzuni.*+

21 Kwa maana kifo kimeingia kupitia madirisha yetu;

Kimeingia ndani ya minara yetu yenye ngome

Ili kuwaondoa watoto barabarani

Na vijana kwenye viwanja vya jiji.’+

22 Sema, ‘Yehova anasema hivi:

“Maiti za watu zitaanguka kama mbolea juu ya ardhi shambani,

Kama safu ya miganda ya nafaka iliyotoka kukatwa na mvunaji,

Bila mtu wa kuikusanya.”’”+

23 Yehova anasema hivi:

“Mtu mwenye hekima asijigambe kwa sababu ya hekima yake;+

Mtu mwenye nguvu asijigambe kwa sababu ya nguvu zake;

Na tajiri asijigambe kwa sababu ya utajiri wake.”+

24 “Lakini yule anayejigamba na ajigambe* kwa jambo hili:

Kwamba ana ufahamu na ujuzi kunihusu,+

Kwamba mimi ni Yehova, Ninayetenda kwa upendo mshikamanifu, haki, na uadilifu duniani,+

Kwa maana ninapendezwa na mambo hayo,”+ asema Yehova.

25 “Tazama! Siku zinakuja,” asema Yehova, “nami nitamwadhibu* kila mtu aliyetahiriwa lakini bado hajatahiriwa,+ 26 yaani, Misri+ na Yuda+ na Edomu+ na Waamoni+ na Moabu+ na wale wote wanaonyoa nywele pembeni mwa vichwa vyao ambao wanakaa nyikani;+ kwa maana mataifa yote hayajatahiriwa, na watu wote wa nyumba ya Israeli hawajatahiriwa moyoni.”+

10 Sikieni neno ambalo Yehova amesema dhidi yenu, enyi watu wa nyumba ya Israeli. 2 Yehova anasema hivi:

“Msijifunze njia ya mataifa,+

Wala msihofu ishara za mbinguni

Kwa sababu mataifa yanazihofu.+

 3 Kwa maana desturi za mataifa ni udanganyifu.*

Ni mti tu wa msituni uliokatwa,

Uliochongwa kwa mikono ya fundi kwa kifaa chake.*+

 4 Wanaupamba kwa fedha na dhahabu+

Wanaupigilia misumari kwa nyundo ili usianguke.+

 5 Kama sanamu ya kufukuza ndege katika shamba la matango, haziwezi kuzungumza;+

Lazima zibebwe, kwa maana haziwezi kutembea.+

Msiziogope kwa maana haziwezi kuwadhuru,

Wala haziwezi kufanya jambo lolote jema.”+

 6 Hakuna yeyote aliye kama wewe, Ee Yehova.+

Wewe ni mkuu, na jina lako ni kuu na lenye nguvu.

 7 Ni nani asiyepaswa kukuogopa, Ee Mfalme wa mataifa,+ kwa maana ni jambo linalofaa;

Kwa sababu kati ya watu wote wenye hekima wa mataifa na kati ya falme zao zote,

Hakuna yeyote yule aliye kama wewe.+

 8 Wote hawatumii akili nao ni wajinga.+

Mafundisho kutoka kwa mti ni udanganyifu* mtupu.+

 9 Mabamba ya fedha huletwa kutoka Tarshishi+ na dhahabu kutoka Ufazi,

Kazi ya fundi, ya mikono ya mhunzi.

Mavazi yao ni nyuzi za bluu na sufu ya zambarau.

Vyote hutengenezwa na wafanyakazi stadi.

10 Lakini kwa kweli Yehova ni Mungu.

Yeye ndiye Mungu aliye hai+ na Mfalme wa milele.+

Kwa sababu ya ghadhabu yake dunia itatetemeka,+

Na hakuna taifa litakalostahimili shutuma yake.

11 * Waambieni hivi:

“Miungu ambayo haikuumba mbingu na dunia

Itaangamia kutoka duniani na kutoka chini ya hizi mbingu.”+

12 Yeye ndiye Muumba wa dunia kwa nguvu zake,

Yule aliyeiimarisha ardhi inayozaa kwa hekima yake+

Na aliyezitandaza mbingu kwa uelewaji wake.+

13 Anapofanya sauti yake isikike,

Maji yaliyo mbinguni husukasuka,+

Naye huyafanya mawingu yapande* kutoka kwenye miisho ya dunia.+

Hutengeneza radi* kwa ajili ya mvua,

Naye huutoa upepo katika maghala yake.+

14 Kila mtu anatenda bila kutumia akili na bila ujuzi.

Kila fundi wa chuma ataaibishwa kwa sababu ya sanamu ya kuchongwa;+

Kwa maana sanamu yake ya chuma* ni uwongo,

Nazo hazina roho* ndani yake.+

15 Sanamu hizo ni udanganyifu,* kazi ya mzaha.+

Siku yao ya hukumu itakapofika, zitaangamia.

16 Fungu la Yakobo si kama vitu hivyo,

Kwa maana Yeye ndiye aliyeumba kila kitu,

Na Israeli ndiyo fimbo ya urithi wake.+

Yehova wa majeshi ndilo jina lake.+

17 Kusanya mzigo wako kutoka ardhini,

Ewe mwanamke uliyezingirwa.

18 Kwa maana Yehova anasema hivi:

“Tazama, ninawatupa* nje wakaaji wa dunia wakati huu,+

Nami nitawafanya wataabike.”

19 Ole wangu kwa sababu ya jeraha langu!*+

Kidonda changu hakiwezi kupona.

Nami nilisema: “Kwa hakika huu ni ugonjwa wangu, na lazima niuvumilie.

20 Hema langu limeharibiwa, na kamba zangu zote za mahema zimekatwa.+

Wanangu wameniacha na hawapo tena.+

Hakuna yeyote aliyebaki wa kulitandaza hema langu au kuviinua vitambaa vyangu vya mahema.

21 Kwa maana wachungaji wametenda kwa upumbavu,+

Wala hawajatafuta ushauri kutoka kwa Yehova.+

Ndiyo sababu hawajatenda kwa ufahamu,

Na kondoo wao wote wametawanyika.”+

22 Sikiliza! Habari! Inakuja!

Kishindo kikubwa kutoka nchi ya kaskazini,+

Ili kuyafanya majiji ya Yuda yawe ukiwa, mapango ya mbwamwitu.+

23 Ninajua vema, Ee Yehova, kwamba njia ya mwanadamu haimo katika uwezo wake.

Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.+

24 Nirekebishe, Ee Yehova, kulingana na hukumu,

Lakini si katika hasira yako,+ usije ukanimaliza.+

25 Yamwagie ghadhabu yako mataifa yanayokupuuza+

Na familia ambazo haziliitii jina lako.

Kwa maana wamemnyafua Yakobo,+

Naam, wamemnyafua na kumwangamiza kabisa,+

Nao wameifanya nchi yake ukiwa.+

11 Hili ndilo neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Yehova, likisema: 2 “Enyi watu, sikieni maneno ya agano hili!

“Watangazie* maneno haya watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu, 3 nawe uwaambie, ‘Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: “Amelaaniwa mtu asiyetii maneno ya agano hili,+ 4 niliyowaamuru mababu zenu siku niliyowatoa nchini Misri,+ kutoka katika tanuru la kuyeyushia chuma,+ nikisema, ‘Tiini sauti yangu, nanyi mfanye mambo yote ninayowaamuru; nanyi mtakuwa watu wangu nami nitakuwa Mungu wenu,+ 5 ili nitimize kiapo nilichowaapia mababu zenu, kwamba nitawapa nchi inayotiririka maziwa na asali,+ kama ilivyo leo hii.’”’”

Nami nikajibu: “Amina,* Ee Yehova.”

6 Kisha Yehova akaniambia: “Tangaza maneno haya yote katika majiji ya Yuda na kwenye barabara za Yerusalemu: ‘Sikieni maneno ya agano hili, na myatekeleze. 7 Kwa maana niliwaonya vikali mababu zenu siku niliyowatoa nchini Misri na mpaka leo hii, niliwaonya tena na tena:* “Tiini sauti yangu.”+ 8 Lakini hawakusikiliza wala kutega sikio lao; badala yake, kila mmoja wao aliendelea kuufuata kwa ukaidi moyo wake mwovu.+ Basi nikawaadhibu kulingana na maneno yote ya agano hili niliyowaamuru wafuate, lakini walikataa kuyatekeleza.’”

9 Kisha Yehova akaniambia: “Kuna njama kati ya watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu. 10 Wameyarudia makosa ya mababu zao wa zamani, waliokataa kutii maneno yangu.+ Wao pia wameifuata miungu mingine na kuiabudu.+ Watu wa nyumba ya Israeli na wa nyumba ya Yuda wamevunja agano langu nililofanya pamoja na mababu zao.+ 11 Kwa hiyo Yehova anasema hivi: ‘Ninawaletea msiba+ ambao hawataweza kuuepuka. Watakaponiomba msaada, sitawasikiliza.+ 12 Kisha majiji ya Yuda na wakaaji wa Yerusalemu wataenda kwa miungu wanayoitolea dhabihu* na kuomba msaada,+ lakini kwa vyovyote vile haitawaokoa watakapopatwa na msiba. 13 Kwa maana miungu yenu imekuwa mingi kama majiji yenu, enyi watu wa Yuda, nanyi mmekitengenezea kitu cha aibu* madhabahu nyingi kama barabara zilizo Yerusalemu, madhabahu za kumtolea dhabihu Baali.’+

14 “Lakini wewe,* usisali kwa ajili ya watu hawa. Usipaze kilio au kusali kwa ajili yao,+ kwa maana sitasikiliza watakaponililia kwa sababu ya msiba wao.

15 Mpendwa wangu ana haki gani ya kuwa katika nyumba yangu

Wakati watu wengi wametekeleza njama nyingi za uovu?

Je, kwa nyama takatifu* watauzuia msiba utakapokujia?

Je, utafurahi wakati huo?

16 Wakati fulani Yehova alikuita mzeituni unaositawi,

Maridadi na wenye matunda mazuri.

Kwa sauti yenye mngurumo mkubwa, ameuwasha moto mzeituni huo,

Nao wamevunja matawi yake.

17 “Yehova wa majeshi, Aliyekupanda,+ ametangaza kwamba msiba utakujia wewe kwa sababu ya uovu uliotendwa na watu wa nyumba ya Israeli na wa nyumba ya Yuda, ambao wamenikasirisha kwa kumtolea dhabihu Baali.”+

18 Yehova alinijulisha ili nijue;

Wakati huo ulinionyesha mambo waliyokuwa wakitenda.

19 Nilikuwa kama mwanakondoo mtulivu anayepelekwa machinjioni.

Sikujua kwamba walikuwa wakipanga njama dhidi yangu:+

“Na tuuangamize ule mti na matunda yake,

Na tumkate kabisa kutoka kwenye nchi ya walio hai,

Ili jina lake lisikumbukwe kamwe.”

20 Lakini Yehova wa majeshi huhukumu kwa uadilifu;

Huchunguza mawazo ya ndani kabisa* na pia moyo.+

Acha nione ukiwalipiza kisasi,

Kwa maana nimeileta kesi yangu kwako.

21 Kwa hiyo Yehova anasema hivi dhidi ya watu wa Anathothi+ wanaotaka kukuua* na wanaosema: “Usitabiri katika jina la Yehova,+ la sivyo tutakuua kwa mikono yetu”; 22 kwa hiyo Yehova wa majeshi anasema hivi: “Tazama, nitawaadhibu.* Vijana watakufa kwa upanga,+ na wana wao na mabinti wao watakufa kwa njaa kali.+ 23 Hakuna yeyote atakayebaki kati yao, kwa maana nitawaletea msiba watu wa Anathothi+ katika mwaka wao wa kuadhibiwa.”*

12 Wewe ni mwadilifu, Ee Yehova,+ ninapokuletea malalamishi yangu,

Ninapozungumza nawe kuhusu mambo ya haki.

Lakini kwa nini njia ya waovu imefanikiwa,+

Na kwa nini watu wenye hila hawana wasiwasi?

 2 Uliwapanda, nao wametia mizizi.

Wamekua na kuzaa matunda.

Wewe uko kwenye midomo yao, lakini uko mbali na mawazo yao ya ndani kabisa.*+

 3 Lakini unanijua vema, Ee Yehova,+ unaniona;

Umeuchunguza moyo wangu na kuupata ukiwa katika muungano nawe.+

Waweke kando kama kondoo wa kuchinjwa,

Na uwatenge kwa ajili ya siku ya kuuawa.

 4 Nchi itaendelea kunyauka mpaka lini

Na majani ya kila uwanja kukauka?+

Kwa sababu ya uovu wa wale wanaokaa ndani yake,

Wanyama na ndege wamefagiliwa mbali.

Kwa maana wamesema: “Haoni kitakachotupata.”

 5 Ikiwa unachoka unapokimbia pamoja na watu waendao kwa miguu,

Unawezaje kushindana mbio na farasi?+

Hata kama una uhakika katika nchi ya amani,

Itakuwaje kwako kati ya vichaka vikubwa kando ya Yordani?

 6 Kwa maana hata ndugu zako mwenyewe, nyumba ya baba yako mwenyewe,

Wamekutendea kwa hila.+

Wamelia kwa sauti kubwa dhidi yako.

Usiwe na imani nao,

Hata wakikuambia mambo mema.

 7 “Nimeiacha nyumba yangu;+ nimeuacha urithi wangu.+

Mpendwa wangu nimpendaye sana* nimemtia mikononi mwa maadui wake.+

 8 Urithi wangu umekuwa kwangu kama simba msituni.

Amenguruma dhidi yangu.

Kwa hiyo nimemchukia.

 9 Urithi wangu ni kama ndege anayewinda mwenye rangi nyingi;*

Ndege wengine wanaowinda wanamzunguka na kumshambulia.+

Njooni, kusanyikeni pamoja, ninyi nyote wanyama wa mwituni,

Njooni mle.+

10 Wachungaji wengi wameliharibu shamba langu la mizabibu;+

Wamelikanyaga-kanyaga shamba langu.+

Wameligeuza shamba langu linalotamanika kuwa nyika yenye ukiwa.

11 Limekuwa ukiwa;

Limenyauka;*

Limekuwa mahame mbele zangu.+

Nchi yote imefanywa kuwa mahame,

Lakini hakuna mtu anayelitia jambo hilo moyoni.+

12 Waangamizaji wamekuja kwenye vijia vyote vya nyikani vilivyokanyagwa sana,

Kwa maana upanga wa Yehova unanyafua kuanzia mwisho mmoja wa nchi mpaka mwisho wa pili.+

Hakuna amani kwa yeyote.*

13 Wamepanda ngano, lakini wamevuna miiba.+

Wamejichosha wenyewe, lakini hawajapata faida yoyote.

Wataona aibu kwa sababu ya mazao yao

Kwa sababu ya hasira ya Yehova inayowaka.”

14 Yehova anasema hivi dhidi ya majirani wangu wote waovu, wanaogusa urithi niliowamilikisha watu wangu Waisraeli:+ “Tazama, ninawang’oa kutoka kwenye nchi yao,+ nami nitawang’oa watu wa nyumba ya Yuda kutoka kati yao. 15 Lakini baada ya kuwang’oa, nitawaonyesha tena rehema na kumrudisha kila mmoja wao kwenye urithi wake na kwenye ardhi yake.”

16 “Na wakihakikisha kwamba wanajifunza njia za watu wangu na kuapa kwa jina langu, ‘Kwa hakika kama Yehova anavyoishi!’ kama walivyowafundisha watu wangu kuapa kwa jina la Baali, ndipo watakapojengwa miongoni mwa watu wangu. 17 Lakini wakikataa kutii, mimi pia nitaling’oa taifa hilo, nitaling’oa na kuliangamiza,” asema Yehova.+

13 Yehova aliniambia hivi: “Nenda ukajinunulie mshipi wa kitani ujifunge kiunoni, lakini usiutie ndani ya maji.” 2 Basi nikanunua mshipi kulingana na neno la Yehova nikajifunga kiunoni. 3 Na neno la Yehova likanijia mara ya pili likisema: 4 “Uchukue mshipi ulionunua ambao umejifunga, nawe uinuke na kwenda kwenye Mto Efrati, uufiche huko katika mpasuko wa jabali.” 5 Basi nikaenda, nikauficha kando ya Mto Efrati, kama Yehova alivyoniamuru.

6 Lakini baada ya siku nyingi Yehova akaniambia: “Inuka, nenda kwenye Mto Efrati, uchukue kutoka huko ule mshipi niliokuamuru uufiche huko.” 7 Basi nikaenda kwenye Mto Efrati, nikachimba na kuuchukua ule mshipi kutoka mahali nilipouficha, nami nikaona kwamba mshipi huo ulikuwa umeharibika; haukufaa kabisa.

8 Kisha neno la Yehova likanijia likisema: 9 “Yehova anasema hivi, ‘Hivyo ndivyo nitakavyokiharibu kiburi cha Yuda na kiburi kingi cha Yerusalemu.+ 10 Watu hawa waovu wanaokataa kutii maneno yangu,+ wanaofuata kwa ukaidi moyo wao wenyewe,+ na wanaofuata miungu mingine, wakiiabudu na kuiinamia, watakuwa kama mshipi huu usiofaa kabisa.’ 11 ‘Kwa maana kama vile mshipi unavyoshikamana na kiuno cha mtu, ndivyo nilivyowafanya watu wote wa nyumba ya Israeli na watu wote wa nyumba ya Yuda washikamane nami,’ asema Yehova, ‘ili wawe watu wangu,+ jina,+ sifa, na kitu maridadi kwangu. Lakini hawakutii.’+

12 “Nawe unapaswa pia kuwapa ujumbe huu: ‘Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: “Kila mtungi mkubwa unapaswa kujazwa divai.”’ Nao watakujibu, ‘Je, tayari hatujui kwamba kila mtungi mkubwa unapaswa kujazwa divai?’ 13 Kisha uwaambie, ‘Yehova anasema hivi: “Tazama, ninawajaza ulevi wakaaji wote wa nchi hii,+ wafalme wanaoketi kwenye kiti cha ufalme cha Daudi, makuhani na manabii, na wakaaji wote wa Yerusalemu. 14 Nami nitawaponda kwa kuwagonganisha mtu na mwenzake, baba na wana pia,” asema Yehova.+ “Sitawahurumia wala kuwasikitikia kamwe wala kuwaonyesha rehema yoyote; hakuna kitakachonizuia nisiwaangamize.”’+

15 Sikieni na mtege sikio.

Msiwe na kiburi, kwa maana Yehova amesema.

16 Mtukuzeni Yehova Mungu wenu

Kabla hajaleta giza

Na kabla miguu yenu haijajikwaa kwenye milima jioni.

Mtatumaini kupata nuru,

Lakini ataleta kivuli kizito;

Ataigeuza nuru iwe giza zito.+

17 Nanyi mkikataa kusikiliza,

Nitalia* kisiri kwa sababu ya kiburi chenu.

Nitatoa machozi mengi, na macho yangu yatabubujika machozi,+

Kwa sababu kondoo wa Yehova+ wamechukuliwa mateka.

18 Mwambie mfalme na mama malkia,+ ‘Ketini mahali pa chini,

Kwa maana taji lenu maridadi litaanguka kutoka kwenye vichwa vyenu.’

19 Majiji ya kusini yamefungwa,* na hakuna mtu wa kuyafungua.

Watu wote wa Yuda wamepelekwa uhamishoni, wamepelekwa kabisa uhamishoni.+

20 Inua macho yako uwaone wale wanaokuja kutoka kaskazini.+

Liko wapi kundi ulilopewa, kondoo wako maridadi?+

21 Utasema nini adhabu yako itakapofika

Kutoka kwa marafiki wako wa karibu uliowafundisha tangu mwanzo?+

Je, hutashikwa na uchungu wa kuzaa, kama wa mwanamke anayezaa?+

22 Nawe ukijiuliza moyoni mwako, ‘Kwa nini nimepatwa na mambo haya?’+

Umevuliwa nguo yako kwa sababu ya kosa lako kubwa+

Na visigino vyako vimetendewa kikatili.

23 Je, Mkushi* anaweza kuibadili ngozi yake, au chui madoa yake?+

Kama inawezekana, basi mnaweza kutenda mema,

Ninyi mliozoezwa kutenda uovu.

24 Basi nitawatawanya kama nyasi kavu zinazopeperushwa na upepo wa jangwani.+

25 Hii ndiyo kura yako, fungu nililokupimia,” asema Yehova,

“Kwa sababu umenisahau+ nawe unautumaini uwongo.+

26 Kwa hiyo, nitainua nguo yako juu ya uso wako,

Na aibu yako itaonekana,+

27 Matendo yako ya uzinzi+ na kilio chako cha uchu,

Ukahaba wako uliopotoka.*

Juu ya vilima, katika mashamba,

Nimeyaona matendo yako yanayochukiza.+

Ole wako, Ee Yerusalemu!

Utaendelea kuwa mchafu mpaka lini?”+

14 Hili ndilo neno la Yehova lililomjia Yeremia kuhusu ukame:+

 2 Yuda inaomboleza,+ na malango yake yamefifia.

Yamehuzunika na kuzama ardhini,

Na kilio kinapanda juu kutoka Yerusalemu.

 3 Na mabwana wao wanawatuma watumishi wao* walete maji.

Wanaenda kwenye visima* lakini hawapati maji.

Wanarudi vyombo vyao vikiwa vitupu.

Wameaibika na kukata tamaa,

Nao wanavifunika vichwa vyao.

 4 Kwa sababu udongo umepasuka,

Kwa maana hakuna mvua nchini,+

Wakulima wametamauka na kuvifunika vichwa vyao.

 5 Hata paa jike aliye porini anamwacha mtoto wake mchanga

Kwa sababu hakuna nyasi.

 6 Punda wa mwituni wanasimama kwenye vilima vitupu.

Wanahemahema kama mbwamwitu;

Macho yao yanadhoofika kwa sababu hakuna majani.+

 7 Ingawa makosa yetu yanatushtaki,

Ee Yehova, tenda kwa ajili ya jina lako.+

Kwa maana matendo yetu ya ukosefu wa uaminifu ni mengi,+

Nasi tumekutendea dhambi.

 8 Ee tumaini la Israeli, Mwokozi wake+ wakati wa taabu,

Kwa nini wewe ni kama mgeni nchini,

Kama msafiri alalaye usiku mmoja tu?

 9 Kwa nini wewe ni kama mtu anayeshangaa,

Kama mwanamume mwenye nguvu asiyeweza kuokoa?

Kwa maana uko miongoni mwetu, Ee Yehova,+

Nasi tumeitwa kwa jina lako.+

Usituache.

10 Yehova anasema hivi kuhusu watu hawa: “Wanapenda kutangatanga;+ hawajaizuia miguu yao.+ Basi Yehova hafurahishwi nao.+ Sasa atalikumbuka kosa lao, naye atawaadhibu* kwa sababu ya dhambi zao.”+

11 Kisha Yehova akaniambia: “Usisali kwamba watu hawa wapate mema.+ 12 Wanapofunga, sisikilizi sihi zao,+ na wanapotoa dhabihu nzima za kuteketezwa na matoleo ya nafaka, siyafurahii,+ kwa maana nitawaangamiza kwa upanga, kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari.”+

13 Ndipo nikasema: “Ole wangu, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Tazama, manabii wanawaambia, ‘Hamtaona upanga, wala hamtakumbwa na njaa kali, bali nitawapa amani ya kweli mahali hapa.’”+

14 Kisha Yehova akaniambia: “Manabii wanatabiri uwongo katika jina langu.+ Sikuwatuma wala kuwaamuru wala kuzungumza nao.+ Wanawatabiria ninyi maono ya uwongo na uaguzi* usiofaa kitu na udanganyifu wa moyo wao wenyewe.+ 15 Kwa hiyo mimi Yehova ninasema hivi kuhusu manabii wanaotabiri katika jina langu ingawa sikuwatuma, na wanaosema hakuna upanga wala njaa kali itakayokuja katika nchi hii: ‘Manabii hao wataangamia kwa upanga na kwa njaa kali.+ 16 Na watu wanaotabiriwa mambo hayo watatupwa katika barabara za Yerusalemu kwa sababu ya njaa kali na upanga, na hakuna yeyote atakayewazika+—wao, wake zao, wana wao, au mabinti wao—kwa maana nitawamwagia msiba wanaostahili.’+

17 “Unapaswa kuwaambia neno hili,

‘Macho yangu na yabubujike machozi usiku na mchana, yasiishe,+

Kwa maana bikira, binti ya watu wangu amepondwa kabisa na kuvunjwa,+

Kwa jeraha baya sana.

18 Nikienda shambani na kutazama,

Ninawaona wale waliouawa kwa upanga!+

Na nikiingia jijini,

Ninayaona magonjwa yaliyoletwa na njaa kali!+

Kwa maana nabii na kuhani wamezunguka katika nchi wasiyoijua.’”+

19 Je, umeikataa Yuda kabisa, au, je, umelichukia* Sayuni kabisa?+

Kwa nini umetupiga, hivi kwamba hatuwezi kupona?+

Tulitumaini kupata amani, lakini hakuna jambo lolote jema lililokuja,

Wakati wa kuponywa, lakini kuna hofu!+

20 Tunatambua uovu wetu, Ee Yehova,

Na kosa la mababu zetu,

Kwa maana tumekutendea dhambi.+

21 Kwa ajili ya jina lako, usitukatae;+

Usikidharau kiti chako cha ufalme chenye utukufu.

Kumbuka, nawe usivunje agano lako pamoja nasi.+

22 Je, kuna sanamu yoyote kati ya sanamu za ubatili za mataifa inayoweza kuleta mvua,

Au, je, hata mbingu zinaweza kuleta mvua zenyewe?

Je, si Wewe peke yako, Ee Yehova Mungu wetu?+

Nasi tunakutumaini,

Kwa maana wewe peke yako ndiye uliyefanya mambo hayo yote.

15 Kisha Yehova akaniambia: “Hata kama Musa na Samweli wangekuwa wamesimama mbele zangu,+ singewaonyesha kibali* watu hawa. Wafukuze kutoka mbele zangu. Waache waende. 2 Nao wakikuuliza, ‘Twende wapi?’ unapaswa kuwaambia, ‘Yehova anasema hivi:

“Yeyote aliyekusudiwa kufa kwa ugonjwa unaoua, na afe kwa ugonjwa unaoua!

Yeyote aliyekusudiwa kufa kwa upanga, na afe kwa upanga!+

Yeyote aliyekusudiwa kufa kwa njaa kali, na afe kwa njaa kali!

Na yeyote aliyekusudiwa kwenda utekwani, na aende utekwani!”’+

3 “‘Nami nitawaletea misiba minne,’*+ asema Yehova, ‘upanga ili kuua, mbwa ili kukokota, na ndege wa angani na wanyama wa duniani ili kula na kuharibu.+ 4 Nami nitawafanya wawe kitu cha kutisha kwa falme zote za dunia+ kwa sababu ya Manase mwana wa Hezekia, mfalme wa Yuda, kwa sababu ya mambo aliyofanya Yerusalemu.+

 5 Ni nani atakayekuhurumia, Ee Yerusalemu,

Ni nani atakayekusikitikia,

Na ni nani atakayesimama ili kuuliza kuhusu hali yako?’

 6 ‘Umeniacha mimi,’ asema Yehova.+

‘Unaendelea kunigeuzia mgongo.*+

Basi nitaunyoosha mkono wangu dhidi yako na kukuangamiza.+

Nimechoka kukuhurumia.*

 7 Nami nitawapepeta kwa uma kwenye malango ya nchi.

Nitawaua watoto wao.+

Nitawaangamiza watu wangu,

Kwa sababu wanakataa kuziacha njia zao.+

 8 Wajane wao watakuwa wengi mbele zangu kuliko mchanga wa bahari.

Nitaleta mwangamizaji dhidi yao wakati wa adhuhuri, dhidi ya akina mama na vijana.

Nitawaletea wasiwasi na hofu kwa ghafla.

 9 Mwanamke aliyezaa watoto saba amedhoofika;

Anapumua* kwa shida.

Jua lake limetua wakati bado ni mchana,

Na kusababisha aibu na fedheha.’*

‘Na wachache waliobaki kati yao

Nitawaacha waangamizwe kwa upanga na maadui wao,’ asema Yehova.”+

10 Ole wangu, ewe mama yangu, kwa sababu ulinizaa,+

Mtu anayegombana na kuzozana daima na nchi yote.

Sijamkopesha mtu wala kukopeshwa;

Lakini wote wananilaani.

11 Yehova alisema: “Kwa hakika nitakuhudumia ili upate mema;

Kwa hakika nitakusaidia wakati wa msiba,

Wakati wa taabu dhidi ya adui.

12 Je, kuna yeyote anayeweza kuvunja chuma vipandevipande,

Chuma kutoka kaskazini, na shaba?

13 Nitatoa mali zako na hazina zako ili ziporwe,+

Bila malipo, kwa sababu ya dhambi zako zote katika maeneo yako yote.

14 Nitawapatia maadui wenu

Wazipeleke katika nchi msiyoijua.+

Kwa maana moto umewashwa kwa hasira yangu.

Nao unawaka dhidi yenu.”+

15 Wewe unajua, Ee Yehova,

Nikumbuke na unikazie fikira.

Nilipizie kisasi wanaonitesa.+

Usiache niangamie* kwa sababu wewe hukasiriki upesi.

Ujue kwamba ninabeba shutuma hii kwa sababu yako.+

16 Maneno yako yalipatikana, nami nikayala;+

Na neno lako likawa furaha na shangwe ya moyo wangu,

Kwa maana nimeitwa kwa jina lako, Ee Yehova Mungu wa majeshi.

17 Siketi pamoja na watu wanaopenda raha na kushangilia.+

Kwa sababu mkono wako uko juu yangu, ninaketi peke yangu,

Kwa maana umenijaza ghadhabu.*+

18 Kwa nini maumivu yangu ni ya kudumu na jeraha langu haliponi?

Linakataa kupona.

Je, utakuwa kwangu kama chanzo cha maji cha udanganyifu,

Ambacho hakiwezi kutegemeka?

19 Kwa hiyo Yehova anasema hivi:

“Ukirudi, basi nitakurudisha,

Nawe utasimama mbele zangu.

Ikiwa utatenganisha kilicho na thamani kutoka kwa kisicho na thamani,

Utakuwa kama kinywa changu mwenyewe.*

Watalazimika kuja kwako,

Lakini wewe hutaenda kwao.”

20 “Ninakufanya kuwa ukuta wa shaba wenye ngome kwa watu hawa.+

Kwa hakika watapigana nawe,

Lakini hawatakushinda,+

Kwa maana mimi niko pamoja nawe, ili nikuokoe na kukukomboa,” asema Yehova.

21 “Nami nitakuokoa kutoka mikononi mwa watu waovu

Na kukukomboa kutoka mikononi mwa watu wakatili.”

16 Na neno la Yehova likanijia tena, likisema: 2 “Usioe mke, wala usiwe na wana na mabinti mahali hapa. 3 Kwa maana Yehova anasema hivi kuhusu wana na mabinti wanaozaliwa hapa na kuhusu mama zao wanaowazaa na kuhusu baba zao wanaowazaa katika nchi hii: 4 ‘Watakufa kwa magonjwa hatari,+ lakini hakuna atakayewaombolezea wala kuwazika; watakuwa kama mbolea kwenye ardhi.+ Wataangamia kwa upanga na kwa njaa kali,+ na maiti zao zitakuwa chakula cha ndege wa angani na wanyama wa duniani.’

 5 “Kwa maana Yehova anasema hivi:

‘Usiingie katika nyumba ambamo waombolezaji wanafanya karamu,

Wala usiende kuomboleza au kuwapa pole,’+

‘Kwa maana nimewaondolea watu hawa amani yangu,’ asema Yehova,

‘Pamoja na upendo wangu mshikamanifu na rehema.+

 6 Wakubwa kwa wadogo watakufa katika nchi hii.

Hawatazikwa,

Hakuna mtu atakayewaombolezea,

Wala hakuna mtu atakayejikatakata wala kujitia upara kwa ajili yao.*

 7 Na hakuna mtu atakayewapa chakula wale wanaoomboleza,

Ili kuwafariji baada ya kufiwa;

Wala hakuna yeyote atakayewapa kikombe cha faraja

Ili wanywe kwa sababu ya kumpoteza baba yao au mama yao.

 8 Nawe usiingie katika nyumba ya karamu

Kuketi pamoja nao ili kula na kunywa.’

9 “Kwa maana Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Mahali hapa, katika siku zenu na mbele ya macho yenu wenyewe, nitazikomesha sauti za furaha na shangwe, sauti ya bwana harusi na sauti ya bibi harusi.’+

10 “Utakapowaambia watu hawa maneno haya yote, watakuuliza, ‘Kwa nini Yehova amesema kwamba tutapatwa na msiba wote huu mkubwa? Tumemtendea Yehova Mungu wetu kosa gani na dhambi gani?’+ 11 Utawajibu, ‘“Kwa sababu mababu zenu waliniacha,”+ asema Yehova, “nao waliendelea kuifuata miungu mingine na kuiabudu na kuiinamia.+ Lakini waliniacha mimi, nao hawakuishika sheria yangu.+ 12 Nanyi mmetenda mambo mabaya zaidi kuliko mababu zenu,+ na kila mmoja wenu anaufuata ukaidi wa moyo wake mwovu badala ya kunitii.+ 13 Basi nitawatupa nje ya nchi hii mpaka kwenye nchi ambayo wala ninyi wala mababu zenu hawakuijua,+ na huko mtalazimika kuiabudu miungu mingine mchana na usiku,+ kwa sababu sitawaonyesha kibali.”’

14 “‘Hata hivyo, siku zinakuja,’ asema Yehova, ‘wakati ambapo hawatasema tena: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, aliyewatoa watu wa Israeli nchini Misri!”+ 15 badala yake watasema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, aliyewatoa watu wa Israeli katika nchi ya kaskazini na katika nchi zote ambako alikuwa amewatawanya!” nami nitawarudisha katika nchi yao, niliyowapa mababu zao.’+

16 ‘Tazama, ninawaita wavuvi wengi,’ asema Yehova,

‘Nao watawavua.

Na baada ya hapo nitawaita wawindaji wengi,

Nao watawawinda kwenye kila mlima na kila kilima

Na kutoka kwenye mipasuko ya majabali.

17 Kwa maana macho yangu yanaona kila kitu wanachofanya.*

Hawajafichwa kutoka mbele zangu,

Wala kosa lao halijafichwa kutoka mbele ya macho yangu.

18 Kwanza, nitalipa kiwango kamili kinachostahili kosa lao na dhambi yao,+

Kwa maana wameitia unajisi nchi yangu kwa mifano isiyo hai ya* sanamu zao zinazochukiza

Nao wameujaza urithi wangu mambo yao yanayochukiza.’”+

19 Ee Yehova, nguvu zangu na ngome yangu,

Kimbilio langu katika siku ya taabu,+

Mataifa yatakuja kwako kutoka kwenye miisho ya dunia,

Nayo yatasema: “Mababu zetu walirithi uwongo mtupu,

Ubatili na vitu visivyofaa kitu ambavyo havina faida yoyote.”+

20 Je, mwanadamu anaweza kujitengenezea miungu

Wakati kwa kweli hiyo si miungu?+

21 “Basi nitawafanya wajue,

Wakati huu nitawafanya wajue nguvu zangu na uwezo wangu,

Nao watalazimika kujua kwamba jina langu ni Yehova.”

17 “Dhambi ya Yuda imeandikwa kwa kalamu ya chuma.

Imechongwa kwa ncha ya almasi juu ya bamba la moyo wao

Na juu ya pembe za madhabahu zao,

 2 Huku wana wao wakikumbuka madhabahu zao na miti yao mitakatifu*+

Kando ya mti wenye majani mengi, juu ya vilima virefu,+

 3 Juu ya milima katika maeneo yaliyo wazi ya mashambani.

Mali zako, hazina zako zote, nitazitoa ili ziporwe+

—Naam, mahali pako pa juu kwa sababu ya dhambi katika maeneo yako yote.+

 4 Utauacha kwa kupenda urithi wako niliokupa.+

Nami nitakufanya uwatumikie maadui wako katika nchi usiyoijua,+

Kwa maana umeiwasha hasira yangu kama moto.*+

Itaendelea kuwaka daima.”

 5 Yehova anasema hivi:

“Amelaaniwa mtu* anayewatumaini wanadamu,+

Anayetegemea nguvu za wanadamu,*+

Na ambaye moyo wake unamwacha Yehova.

 6 Atakuwa kama mti ulio peke yake jangwani.

Hataona mema yatakapokuja,

Lakini atakaa mahali pakavu nyikani,

Katika nchi yenye chumvi ambayo hakuna mtu anayeweza kuishi ndani yake.

 7 Amebarikiwa mtu* anayemtumaini Yehova,

Ambaye uhakika wake uko katika Yehova.+

 8 Atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji,

Unaopeleka mizizi yake kwenye kijito.

Hatatambua joto linapokuja,

Bali majani yake yatasitawi sikuzote.+

Naye hatakuwa na mahangaiko katika mwaka wa ukame,

Wala hataacha kuzaa matunda.

 9 Moyo ni wenye hila* kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.*+

Ni nani anayeweza kuujua?

10 Mimi, Yehova, ninauchunguza moyo,+

Ninakagua mawazo ya ndani kabisa,*

Ili kumpa kila mmoja kulingana na njia zake,

Kulingana na matunda ya matendo yake.+

11 Kama kwale anayekusanya kile ambacho hakutaga,

Ndivyo alivyo mtu anayekusanya utajiri kwa udanganyifu.*+

Atauacha katikati ya maisha yake,

Na mwishowe ataonekana hana akili.”

12 Kiti cha ufalme chenye utukufu, kilichokwezwa tangu mwanzo,

Ndicho mahali petu patakatifu.+

13 Ee Yehova, tumaini la Israeli,

Wote wanaokuacha wataaibishwa.

Wale wanaokuasi* wataandikwa mavumbini,+

Kwa sababu wamemwacha Yehova, chanzo cha maji yaliyo hai.+

14 Niponye, Ee Yehova, nami nitapona.

Niokoe, nami nitaokoka,+

Kwa maana ninakusifu wewe.

15 Tazama! Kuna wale wanaoniambia:

“Neno la Yehova liko wapi?+

Na lije, tafadhali!”

16 Lakini mimi, sikukimbia na kuacha kukufuata ukiwa mchungaji,

Wala sikutamani siku ya msiba.

Unajua vema mambo yote ambayo midomo yangu imesema;

Yote yalitendeka mbele za uso wako!

17 Usiwe tisho kwangu.

Wewe ni kimbilio langu katika siku ya msiba.

18 Wale wanaonitesa na waaibishwe,+

Lakini usiruhusu niaibishwe.

Waache washikwe na hofu,

Lakini usiruhusu nishikwe na hofu.

Ilete siku ya msiba juu yao,+

Nawe uwaponde na kuwaangamiza kabisa.*

19 Yehova aliniambia hivi: “Nenda usimame katika lango la wana wa watu ambalo wafalme wa Yuda huingilia na kutokea, na katika malango yote ya Yerusalemu.+ 20 Nawe unapaswa kuwaambia hivi: ‘Sikieni neno la Yehova, ninyi wafalme wa Yuda, watu wote wa Yuda, na wakaaji wote wa Yerusalemu, mnaoingia kupitia malango haya. 21 Yehova anasema hivi: “Jihadharini, nanyi msibebe mzigo wowote siku ya Sabato wala kuuingiza kupitia malango ya Yerusalemu.+ 22 Hampaswi kutoa mzigo wowote katika nyumba zenu siku ya Sabato; nanyi hampaswi kufanya kazi yoyote.+ Endeleeni kuishika siku ya Sabato ikiwa siku takatifu, kama nilivyowaamuru mababu zenu.+ 23 Lakini hawakusikiliza wala kutega sikio lao, nao wakakataa kwa ukaidi* kutii au kukubali nidhamu.”’+

24 “‘“Hata hivyo, mkinitii kabisa,” asema Yehova, “nanyi msiingize mzigo wowote kupitia malango ya jiji hili siku ya Sabato, nanyi mwendelee kuishika siku ya Sabato ikiwa siku takatifu kwa kutofanya kazi yoyote siku hiyo,+ 25 ndipo wafalme na wakuu wanaoketi kwenye kiti cha ufalme cha Daudi+ wataingia pia kupitia malango ya jiji hili, wakipanda gari na farasi, wao pamoja na wakuu wao, watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu;+ na jiji hili litaendelea kuwa na watu daima. 26 Na watu watakuja kutoka katika majiji ya Yuda, kutoka maeneo yanayozunguka Yerusalemu, kutoka nchi ya Benjamini,+ maeneo ya chini,+ kutoka eneo lenye milima, na kutoka Negebu;* wataleta dhabihu nzima za kuteketezwa,+ dhabihu nyingine,+ matoleo ya nafaka,+ ubani, na dhabihu za shukrani ndani ya nyumba ya Yehova.+

27 “‘“Lakini msiponitii kwa kutoshika siku ya Sabato ikiwa siku takatifu na mkibeba mizigo na kuileta kupitia malango ya Yerusalemu katika siku ya Sabato, nitayawasha moto malango yake, nao hakika utaiteketeza minara yenye ngome ya Yerusalemu+ nao hautazimwa.”’”+

18 Hili ndilo neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Yehova: 2 “Inuka na ushuke mpaka kwenye nyumba ya mfinyanzi,+ na huko nitakuambia maneno yangu.”

3 Basi nikashuka mpaka kwenye nyumba ya mfinyanzi, naye alikuwa akifanya kazi kwenye magurudumu ya mfinyanzi. 4 Lakini chombo alichokuwa akitengeneza kikaharibika mikononi mwake. Basi mfinyanzi akakitengeneza upya kuwa chombo kingine, kama alivyopenda.*

5 Kisha neno la Yehova likanijia likisema: 6 “‘Je, siwezi kuwatendea kama mfinyanzi huyu alivyotenda, enyi watu wa nyumba ya Israeli?’ asema Yehova. ‘Tazama! Kama udongo mikononi mwa mfinyanzi, ndivyo mlivyo mikononi mwangu, enyi watu wa nyumba ya Israeli.+ 7 Wakati wowote nitakaposema kuhusu kung’oa na kubomoa na kuharibu taifa au ufalme,+ 8 na taifa hilo liache uovu wake niliotangaza dhidi yake, mimi pia nitabadili nia yangu* kuhusu msiba niliokusudia kuuleta dhidi yake.+ 9 Lakini wakati wowote ninaposema kuhusu kujenga na kupanda taifa au ufalme, 10 na taifa hilo litende maovu machoni pangu na kukosa kuitii sauti yangu, mimi pia nitabadili nia yangu* kuhusu mema niliyokusudia kulitendea.’

11 “Sasa, tafadhali, waambie watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu, ‘Yehova anasema hivi: “Ninatayarisha* msiba na kupanga njama dhidi yenu. Geukeni, tafadhali, kutoka kwenye njia zenu mbaya, na mrekebishe njia zenu na matendo yenu.”’”+

12 Lakini wakasema: “Hakuna tumaini lolote!+ Kwa maana tutafuata mawazo yetu wenyewe, na kila mmoja wetu atatenda kulingana na ukaidi wa moyo wake mwovu.”+

13 Kwa hiyo Yehova anasema hivi:

“Ulizeni wenyewe, tafadhali, kati ya mataifa.

Ni nani amesikia jambo kama hili?

Bikira wa Israeli ametenda jambo linalochukiza sana.+

14 Je, theluji ya Lebanoni inatoweka kwenye miamba iliyo kwenye miteremko yake?

Au, je, maji baridi yanayotiririka kutoka mbali yatakauka?

15 Lakini watu wangu wamenisahau.+

Kwa maana wanakitolea dhabihu* kitu cha ubatili,+

Nao wanawafanya watu wajikwae katika njia zao, vijia vya kale,+

Ili wapite kwenye barabara za vichochoroni ambazo hazijasawazishwa na ambazo si tambarare,*

16 Ili kuifanya nchi yao kuwa kitu cha kutisha+

Na kitu cha kupigiwa mluzi milele.+

Kila mtu atakayepita kando yake atatazama kwa mshtuko na kutikisa kichwa chake.+

17 Kama upepo wa mashariki, nitawatawanya mbele ya adui.

Nitawaonyesha mgongo, si uso wangu, siku ya msiba wao.”+

18 Nao wakasema: “Njooni, tupange njama dhidi ya Yeremia,+ kwa maana sheria haitatoweka* kutoka kwa makuhani wetu au shauri kutoka kwa watu wenye hekima au neno kutoka kwa manabii. Njooni tumshambulie kwa maneno,* nasi tusisikilize anachosema.”

19 Nitegee sikio, Ee Yehova,

Nawe usikilize wanachosema wapinzani wangu.

20 Je, wema unapaswa kulipwa kwa uovu?

Kwa maana wameuchimbia shimo uhai wangu.*+

Kumbuka jinsi nilivyosimama mbele zako ili kusema mema kuwahusu,

Ili kuwaondolea ghadhabu yako.

21 Basi waache wana wao wapatwe na njaa kali,

Na uwatie mikononi mwa nguvu za upanga.+

Wake zao na wafiwe na watoto na kuwa wajane.+

Wanaume wao na wauawe kwa ugonjwa unaoua,

Vijana wao wauawe kwa upanga vitani.+

22 Kilio na kisikiwe kutoka katika nyumba zao

Utakapowaletea wavamizi kwa ghafla.

Kwa maana wamechimba shimo ili kunikamata

Nao wametega mitego ya kuinasa miguu yangu.+

23 Lakini wewe, Ee Yehova,

Unajua vema njama zao zote za kuniua.+

Usilifunike kosa lao,

Wala usiifute dhambi yao kutoka mbele zako.

Na wakwazike mbele zako+

Utakapowachukulia hatua kwa hasira yako.+

19 Yehova alisema hivi: “Nenda ukanunue chupa ya udongo kwa mfinyanzi.+ Uwachukue baadhi ya wazee wa watu na baadhi ya wazee wa makuhani, 2 nawe uende katika Bonde la Mwana wa Hinomu,+ kwenye njia inayoelekea kwenye Lango la Vigae. Na huko utangaze maneno ninayokuambia. 3 Utasema, ‘Sikieni neno la Yehova, enyi wafalme wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu. Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi:

“‘“Niko karibu kuleta msiba mahali hapa, na masikio ya yeyote anayesikia kuuhusu yatawasha. 4 Ni kwa sababu waliniacha+ na kufanya mahali hapa pasitambuliwe.+ Hapa wanaitolea dhabihu miungu mingine ambayo wao na mababu zao na wafalme wa Yuda hawakuijua, nao wamepajaza mahali hapa damu ya watu wasio na hatia.+ 5 Walijenga mahali pa juu pa Baali ili kuwateketeza motoni wana wao kuwa dhabihu nzima za kuteketezwa kwa Baali,+ jambo ambalo sikuamuru wala kusema na ambalo hata halijawahi kamwe kuingia moyoni mwangu.”’*+

6 “‘“Kwa hiyo tazameni! siku zinakuja,” asema Yehova, “wakati mahali hapa hapataitwa tena Tofethi au Bonde la Mwana wa Hinomu bali Bonde la Mauaji.+ 7 Nitavunja mipango ya Yuda na Yerusalemu mahali hapa, nami nitawaacha maadui wao wawaangamize kwa upanga na pia wataangamizwa kwa mkono wa wale wanaotaka kuwaua.* Nami nitawapa ndege wa angani na wanyama wa duniani maiti zao kuwa chakula chao.+ 8 Nitalifanya jiji hili kuwa kitu cha kutisha na kitu cha kupigiwa mluzi. Kila mtu atakayepita kando yake atatazama kwa mshtuko na kupiga mluzi kwa sababu ya mapigo yake yote.+ 9 Nami nitawafanya wale nyama ya wana wao na ya mabinti wao, nao watakula kila mmoja nyama ya mwenzake, kwa sababu ya kuzingirwa na kukata tamaa watakapobanwa na maadui wao wanaotaka kuwaua.”’*+

10 “Kisha uivunje ile chupa mbele ya macho ya wanaume watakaoenda pamoja nawe, 11 nawe uwaambie, ‘Yehova wa majeshi anasema hivi: “Hivi ndivyo nitakavyowavunja watu hawa na jiji hili, kama mtu anavyovunja chombo cha mfinyanzi hivi kwamba hakiwezi kurekebishwa kamwe; nao watawazika wafu katika Tofethi hivi kwamba hakutakuwa na nafasi zaidi ya kuwazika.”’+

12 “‘Hivyo ndivyo nitakavyopatendea mahali hapa,’ asema Yehova, ‘na wakaaji wake, ili kulifanya jiji hili liwe kama Tofethi. 13 Na nyumba za Yerusalemu na nyumba za wafalme wa Yuda zitakuwa chafu kama mahali hapa, Tofethi,+ naam, nyumba zote ambazo juu ya paa zake walilitolea dhabihu jeshi lote la mbinguni+ na ambako waliimiminia miungu mingine matoleo ya kinywaji.’”+

14 Yeremia aliporudi kutoka Tofethi ambako Yehova alikuwa amemtuma ili atabiri huko, akasimama katika ua wa nyumba ya Yehova na kuwaambia hivi watu wote: 15 “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Tazameni, ninaliletea jiji hili na miji yake yote msiba wote ambao nimetangaza dhidi yake, kwa sababu walikataa kwa ukaidi kuyatii* maneno yangu.’”+

20 Sasa Pashuri mwana wa Imeri, kuhani, ambaye pia alikuwa msimamizi mkuu katika nyumba ya Yehova, alikuwa akisikiliza Yeremia alipokuwa akitabiri mambo hayo. 2 Kisha Pashuri akampiga nabii Yeremia na kumweka katika mikatale+ iliyokuwa kwenye Lango la Juu la Benjamini, lililokuwa katika nyumba ya Yehova. 3 Lakini siku iliyofuata Pashuri alipomtoa Yeremia katika ile mikatale, Yeremia akamwambia:

“Yehova hatakuita tena Pashuri, bali Hofu Kila Upande.+ 4 Kwa maana Yehova anasema hivi: ‘Nitakufanya uwe kitu cha kutia hofu kwako mwenyewe na kwa marafiki wako wote, nao watauawa kwa upanga wa maadui wao huku macho yako yakitazama;+ nami nitawatia watu wote wa Yuda mikononi mwa mfalme wa Babiloni, naye atawapeleka uhamishoni kule Babiloni na kuwaua kwa upanga.+ 5 Nami nitatia mikononi mwa maadui wao utajiri wote wa jiji hili, mali zake zote, vitu vyake vyote vyenye thamani, na hazina zote za wafalme wa Yuda.+ Nao watapora vitu hivyo na kuvichukua na kuvipeleka Babiloni.+ 6 Lakini wewe, Pashuri, na wote wanaoishi katika nyumba yako, mtapelekwa utekwani. Utapelekwa Babiloni na kufia huko, nawe utazikwa huko pamoja na marafiki wako wote, kwa sababu umewatabiria uwongo.’”+

 7 Umenipumbaza, Ee Yehova, nami nikapumbazika.

Ulizitumia nguvu zako kunipinga, nawe ukashinda.+

Nimekuwa kitu cha kuchekwa mchana kutwa;

Kila mtu ananidhihaki.+

 8 Kwa maana kila mara ninapozungumza, lazima nipaze sauti na kutangaza,

“Ukatili na uharibifu!”

Kwa maana neno la Yehova limesababisha nitukanwe na kudhihakiwa siku nzima.+

 9 Basi nikasema: “Sitamtaja tena,

Wala sitasema tena katika jina lake.”+

Lakini moyoni mwangu neno hilo lilikuwa kama moto unaowaka uliofungiwa mifupani mwangu,

Nami nikachoka kulizuia ndani yangu;

Singeweza tena kuvumilia.+

10 Kwa maana nilisikia uvumi mwingi wa uovu;

Hofu ilinizunguka.+

“Mshutumuni; na tumshtumu!”

Kila mtu aliyenitakia amani alisubiri nianguke:+

“Labda atafanya kosa la kipumbavu,

Nasi tutamshinda na kujilipizia kisasi dhidi yake.”

11 Lakini Yehova alikuwa pamoja nami kama shujaa anayetisha.+

Ndiyo sababu wale wanaonitesa watajikwaa nao hawatashinda.+

Wataaibishwa sana, kwa maana hawatafanikiwa.

Fedheha yao ya milele haitasahauliwa.+

12 Lakini wewe, Ee Yehova wa majeshi, unamchunguza mwadilifu;

Unaona mawazo ya ndani kabisa* na pia moyo.+

Acha nione ukiwalipiza kisasi,+

Kwa maana nimeileta kesi yangu kwako.+

13 Mwimbieni Yehova! Msifuni Yehova!

Kwa maana amemwokoa maskini* kutoka mikononi mwa watenda maovu.

14 Ilaaniwe siku niliyozaliwa!

Isibarikiwe siku ambayo mama yangu alinizaa!+

15 Alaaniwe mtu aliyemletea baba yangu habari njema, akisema:

“Umepata mwana, mvulana!”

Na kumfanya ashangilie sana.

16 Mtu huyo na awe kama majiji ambayo Yehova aliyaangamiza bila kughairi.

Na asikie kilio asubuhi na sauti ya king’ora adhuhuri.

17 Kwa nini hakuniua ndani ya tumbo la uzazi,

Ili mama yangu awe kaburi langu

Na tumbo lake liwe na mimba sikuzote?+

18 Kwa nini nilitoka tumboni

Ili kuona taabu na huzuni,

Na kumaliza siku zangu kwa aibu?+

21 Yeremia alipokea neno kutoka kwa Yehova wakati Mfalme Sedekia+ alipomtuma kwake Pashuri+ mwana wa Malkiya na Sefania+ mwana wa Maaseya, kuhani, akiomba hivi: 2 “Tafadhali mwombe Yehova ushauri kwa ajili yetu, kwa sababu Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni anapigana vita dhidi yetu.+ Labda Yehova atatutendea mojawapo ya matendo yake yanayostaajabisha, ili mfalme huyo atuache na kwenda zake.”+

3 Yeremia akawaambia, “Mwambieni Sedekia hivi: 4 ‘Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: “Tazama, ninazigeuza dhidi yenu* silaha za vita zilizo mikononi mwenu, mnazotumia kupigana na mfalme wa Babiloni+ na Wakaldayo wanaowazingira nje ya ukuta. Nami nitawakusanya katikati ya jiji hili. 5 Na mimi mwenyewe nitapigana nanyi+ kwa mkono ulionyooshwa na kwa mkono wenye nguvu, kwa hasira na kwa ghadhabu na kwa ukali mwingi.+ 6 Nitawapiga wakaaji wa jiji hili, mwanadamu na mnyama pia. Watakufa kwa ugonjwa hatari sana.”’+

7 “‘“Baada ya hayo,” asema Yehova, “Nitamtia Mfalme Sedekia wa Yuda na watumishi wake na watu wa jiji hili—wale watakaookoka ugonjwa hatari, upanga, na njaa kali—mikononi mwa Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni, mikononi mwa maadui wao na mikononi mwa wale wanaotaka kuwaua.*+ Atawaua kwa upanga. Hatawasikitikia wala kuwahurumia wala kuwaonyesha rehema yoyote.”’+

8 “Nawe utawaambia watu hawa, ‘Yehova anasema hivi: “Tazameni, ninaweka mbele yenu njia ya uzima na njia ya kifo. 9 Wale watakaobaki katika jiji hili watakufa kwa upanga, kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari. Lakini yeyote atakayetoka na kujisalimisha kwa Wakaldayo wanaowazingira ataendelea kuishi, naye atapata uhai wake* kama nyara.”’*+

10 “‘“Kwa maana nimelikataa* jiji hili nalo litapata msiba wala si mema,”+ asema Yehova. “Litatiwa mikononi mwa mfalme wa Babiloni,+ naye ataliteketeza kwa moto.”+

11 “‘Utawaambia watu wa nyumba ya mfalme wa Yuda: Sikieni neno la Yehova. 12 Enyi watu wa nyumba ya Daudi, Yehova anasema hivi:

“Tekelezeni haki kila asubuhi,

Na mtu anayenyang’anywa, mwokoeni kutoka mikononi mwa mtu laghai,+

Ili ghadhabu yangu isiwake kama moto+

Na kuteketeza bila mtu wa kuuzima

Kwa sababu ya matendo yenu maovu.”’+

13 ‘Tazama, niko dhidi yako, ewe mkaaji wa bondeni,*

Ewe mwamba wa nchi tambarare,’ asema Yehova.

‘Na wewe unayeuliza: “Ni nani atakayeshuka kupigana nasi?

Na ni nani atakayevamia makao yetu?”

14 Nitakufanya uwajibike*

Kulingana na matendo yenu,’+ asema Yehova.

‘Nami nitawasha moto katika msitu wake,

Nao utateketeza vitu vyote vinavyomzunguka.’”+

22 Yehova anasema hivi: “Shuka nyumbani kwa* mfalme wa Yuda, upeleke ujumbe huu. 2 Utasema, ‘Sikia neno la Yehova, ewe mfalme wa Yuda unayeketi juu ya kiti cha ufalme cha Daudi, wewe pamoja na watumishi wako na watu wako, wale wanaoingia kupitia malango haya. 3 Yehova anasema hivi: “Tekelezeni haki na uadilifu. Na mtu anayenyang’anywa, mwokoeni kutoka mikononi mwa mtu laghai. Msimtese mkaaji yeyote mgeni, na msimdhuru yatima yeyote au mjane.+ Nanyi msimwage damu yoyote isiyo na hatia mahali hapa.+ 4 Kwa maana mkijitahidi kufuata neno hili, basi wafalme wanaoketi kwenye kiti cha ufalme cha Daudi+ wataingia kupitia malango ya nyumba hii, wakiwa wamepanda magari na farasi, wao pamoja na watumishi wao na watu wao.”’+

5 “‘Lakini msipoyatii maneno haya, ninaapa kwa nafsi yangu mwenyewe,’ asema Yehova, ‘kwamba nyumba hii itakuwa ukiwa.’+

6 “Kwa maana Yehova anasema hivi kuhusu nyumba ya mfalme wa Yuda,

‘Wewe ni kama Gileadi kwangu,

Kama kilele cha Lebanoni.

Lakini nitakufanya uwe nyika;

Hakuna jiji lako hata moja litakalokaliwa.+

 7 Nami nitawaweka* waangamizaji dhidi yako,

Kila mmoja akiwa na silaha zake.+

Wataikata mierezi yako iliyo bora zaidi

Na kuiangusha ndani ya moto.+

8 Na mataifa mengi yatapita kando ya jiji hili na kila mmoja atamwambia mwenzake: “Kwa nini Yehova alilitendea hivi jiji hili kuu?”+ 9 Nao watajibu: “Kwa sababu waliliacha agano la Yehova Mungu wao na kuiinamia miungu mingine na kuitumikia.”’+

10 “Msimlilie aliyekufa,

Na msimsikitikie.

Badala yake, mlilieni sana yule anayeondoka,

Kwa maana hatarudi tena kuiona nchi alimozaliwa.

11 “Kwa maana Yehova anasema hivi kumhusu Shalumu*+ mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda anayetawala badala ya Yosia+ baba yake, ambaye ameondoka mahali hapa: ‘Hatarudi hapo tena. 12 Kwa maana atakufa mahali walipompeleka uhamishoni, naye hataiona tena nchi hii.’+

13 Ole wake anayejenga nyumba yake bila uadilifu

Na vyumba vyake vya juu bila haki,

Anayemfanya mwanadamu mwenzake amtumikie bure,

Na ambaye anakataa kumlipa malipo yake;+

14 Yule anayesema, ‘Nitajijengea nyumba yenye nafasi kubwa

Yenye vyumba vya juu vyenye nafasi kubwa.

Nitaiwekea madirisha

Nami nitazifunika kuta zake kwa mbao za mierezi na kuipaka rangi nyekundu.’

15 Je, utaendelea kutawala kwa sababu unawashinda wengine kwa kutumia mierezi?

Baba yako pia alikula na kunywa,

Lakini alitenda haki na uadilifu,+

Naye alifanikiwa.

16 Alitetea haki halali ya mwenye kuteseka na maskini,

Basi akafanikiwa.

‘Hiyo ndiyo maana ya kunijua, sivyo?’ asema Yehova.

17 ‘Lakini macho yako na moyo wako unakazia tu faida yako isiyo ya haki,

Kumwaga damu isiyo na hatia,

Na kufanya ulaghai na unyang’anyi.’

18 “Kwa hiyo Yehova anasema hivi kumhusu Yehoyakimu+ mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda,

‘Hawatamwombolezea:

“Aa! ndugu yangu! Aa! dada yangu!”

Hawatamwombolezea:

“Aa! Ewe bwana! Aa! mfalme!”

19 Atazikwa kama anavyozikwa punda,+

Kwa kukokotwa na kutupwa,

Nje ya malango ya Yerusalemu.’+

20 Panda mpaka Lebanoni na upaze kilio,

Paza sauti yako huko Bashani.

Na upaze kilio kutoka Abarimu,+

Kwa maana wapenzi wako wamepondwa.+

21 Nilisema nawe ulipokuwa salama.

Lakini ulisema, ‘Sitatii.’+

Hii imekuwa njia yako tangu ujana wako,

Kwa maana hujaitii sauti yangu.+

22 Upepo utawachunga wachungaji wako wote,+

Na wapenzi wako wataenda utekwani.

Kisha utaaibishwa na kufedheheshwa kwa sababu ya msiba wako wote.

23 Ewe unayekaa Lebanoni,+

Uliye na kiota kati ya mierezi,+

Jinsi utakavyougua uchungu utakapokupata,

Maumivu* kama ya mwanamke anayezaa!”+

24 “‘Kwa hakika kama ninavyoishi,’ asema Yehova, ‘hata kama Konia*+ mwana wa Yehoyakimu,+ mfalme wa Yuda, angekuwa pete ya muhuri kwenye mkono wangu wa kuume, ningekung’oa kutoka hapo! 25 Nami nitakutia mkononi mwa wale wanaotaka kukuua,* mkononi mwa wale unaowaogopa, mkononi mwa Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni, na mkononi mwa Wakaldayo.+ 26 Nami nitakutupa wewe pamoja na mama yako aliyekuzaa katika nchi nyingine ambako hamkuzaliwa, nanyi mtakufa huko. 27 Nao hawatarudi kamwe katika nchi wanayoitamani.*+

28 Je, mtu huyu Konia ni chungu tu kilichodharauliwa na kuvunjika,

Chombo ambacho hakuna mtu anayekitaka?

Kwa nini yeye na wazao wake wameangushwa chini

Na kutupwa katika nchi wasiyoijua?’+

29 Ewe dunia,* dunia, dunia, sikia neno la Yehova.

30 Yehova anasema hivi:

‘Andikeni kwamba mtu huyu hana mtoto,

Kama mtu ambaye hatafanikiwa katika maisha yake,*

Kwa maana hakuna yeyote kati ya wazao wake atakayefanikiwa

Kuketi kwenye kiti cha ufalme cha Daudi na kutawala tena katika Yuda.’”+

23 “Ole wao wachungaji wanaowaangamiza na kuwatawanya kondoo wa malisho yangu!” asema Yehova.+

2 Kwa hiyo Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi dhidi ya wachungaji wanaowachunga watu wangu: “Mmewatawanya kondoo wangu; mliendelea kuwatawanya, nanyi hamjawakazia fikira.”+

“Basi nitawakazia ninyi fikira kwa sababu ya matendo yenu maovu,” asema Yehova.

3 “Kisha nitawakusanya kondoo wangu waliobaki kutoka katika nchi zote ambako nilikuwa nimewatawanya,+ nami nitawarudisha kwenye malisho yao,+ nao watazaana na kuwa wengi.+ 4 Nami nitaweka wachungaji juu yao ambao kwa kweli watawachunga.+ Hawataogopa tena wala kuwa na hofu, na hakuna yeyote atakayekosekana,” asema Yehova.

5 “Tazameni! Siku zinakuja,” asema Yehova, “nitakapomwinulia Daudi chipukizi adilifu.*+ Na mfalme atatawala+ na kuwa na ufahamu na kutekeleza haki na uadilifu katika nchi.+ 6 Katika siku zake Yuda ataokolewa,+ na Israeli atakaa kwa usalama.+ Naye ataitwa jina hili: Yehova Ni Uadilifu Wetu.”+

7 “Hata hivyo, siku zinakuja,” asema Yehova, “wakati ambapo hawatasema tena, ‘Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, aliyewatoa watu wa Israeli nchini Misri!’+ 8 badala yake watasema, ‘Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, aliyewatoa na kuwarudisha wazao wa nyumba ya Israeli kutoka katika nchi ya kaskazini na kutoka katika nchi zote nilizowatawanya,’ nao watakaa katika nchi yao wenyewe.”+

9 Kuhusu manabii:

Moyo wangu umevunjika ndani yangu.

Mifupa yangu yote inatetemeka.

Mimi ni kama mtu aliyelewa

Na kama mtu aliyelemewa na divai,

Kwa sababu ya Yehova na kwa sababu ya maneno yake matakatifu.

10 Kwa maana nchi imejaa wazinzi;+

Kwa sababu ya laana nchi inaomboleza+

Na malisho ya nyikani yamekauka.+

Njia yao ni ya uovu, nao wanatumia vibaya nguvu zao.

11 “Nabii pamoja na kuhani wamechafuliwa.*+

Hata katika nyumba yangu mwenyewe nimeupata uovu wao,”+ asema Yehova.

12 “Basi kijia chao kitakuwa na utelezi na giza,+

Watasukumwa na kuanguka.

Kwa maana nitawaletea msiba

Katika mwaka wa kuwaadhibu,” asema Yehova.

13 “Na kwa manabii wa Samaria+ nimeona jambo linalochukiza sana.

Unabii wao unachochewa na Baali,

Nao wanawapotosha watu wangu Waisraeli.

14 Na kwa manabii wa Yerusalemu nimeona mambo mabaya sana.

Wanafanya uzinzi+ na kutembea katika uwongo;+

Wanawatia moyo* watenda maovu,

Nao hawageuki na kuuacha uovu wao.

Wote ni kama Sodoma kwangu,+

Na wakaaji wake ni kama Gomora.”+

15 Kwa hiyo Yehova wa majeshi anasema hivi dhidi ya manabii hao:

“Tazama, ninawafanya wale pakanga

Na kuwapa maji yenye sumu wanywe.+

Kwa maana kutoka kwa manabii wa Yerusalemu uasi imani umeenea katika nchi yote.”

16 Yehova wa majeshi anasema hivi:

“Msiyasikilize maneno ya manabii wanaowatabiria ninyi.+

Wanawadanganya.*

Wanasema maono ya moyo wao wenyewe,+

Si kutoka katika kinywa cha Yehova.+

17 Wanawaambia tena na tena wale wasioniheshimu,

‘Yehova amesema hivi: “Mtakuwa na amani.”’+

Nao wanamwambia kila mtu anayefuata moyo wake mkaidi,

‘Hutapatwa na msiba wowote.’+

18 Kwa maana ni nani amesimama katika kikundi cha marafiki wa karibu wa Yehova

Ili aone na kulisikia neno lake?

Ni nani amelikazia fikira neno lake ili alisikie?

19 Tazameni! Dhoruba ya upepo ya Yehova italipuka kwa ghadhabu;

Kama tufani inayozunguka, itazunguka ikishuka juu ya kichwa cha waovu.+

20 Hasira ya Yehova haitapoa

Mpaka atakapotekeleza na kutimiza makusudi ya moyo wake.

Mtaelewa jambo hilo waziwazi katika siku za mwisho.

21 Sikuwatuma manabii, lakini walikimbia.

Sikuongea nao, lakini walitabiri.+

22 Lakini ikiwa wangesimama katika kikundi changu cha marafiki wa karibu,

Wangewafanya watu wangu wayasikie maneno yangu

Nao wangewarudisha kutoka kwenye njia yao mbaya na matendo yao maovu.”+

23 “Je, mimi ni Mungu nikiwa karibu tu,” auliza Yehova, “ na si Mungu nikiwa mbali pia?”

24 “Je, mtu yeyote anaweza kujificha mahali pa siri ambapo siwezi kumwona?”+ auliza Yehova.

“Je, mimi sizijazi mbingu na dunia?”+ auliza Yehova.

25 “Nimewasikia manabii wanaotabiri uwongo katika jina langu wakisema, ‘Niliota ndoto! Niliota ndoto!’+ 26 Jambo hili litaendelea mpaka lini katika moyo wa manabii hao, kutabiri uwongo? Wao ni manabii wa udanganyifu wa moyo wao wenyewe.+ 27 Wanakusudia kuwafanya watu wangu walisahau jina langu kupitia ndoto wanazosimuliana, kama baba zao walivyolisahau jina langu kwa sababu ya Baali.+ 28 Nabii aliye na ndoto na asimulie ndoto hiyo, lakini yule aliye na neno langu anapaswa kulisema neno langu kwa ukweli.”

“Nyasi ina uhusiano gani na nafaka?” auliza Yehova.

29 “Je, neno langu si kama moto,”+ auliza Yehova, “na kama nyundo ya chuma inayopasua-pasua jabali?”+

30 “Basi nitawaadhibu manabii,” asema Yehova, “wanaoibiana maneno yangu.”+

31 “Nitawaadhibu manabii,” asema Yehova, “wanaotumia ulimi wao kusema, ‘Anasema hivi!’”+

32 “Nitawaadhibu manabii wa ndoto za uwongo,” asema Yehova, “wanaozisimulia na kuwapotosha watu wangu kwa sababu ya uwongo wao na kujigamba kwao.”+

“Lakini sikuwatuma wala kuwaamuru. Basi hawatawafaidi watu hawa hata kidogo,”+ asema Yehova.

33 “Na watu hawa au nabii au kuhani akiwauliza, ‘Mzigo* wa Yehova ni nini?’ mtawajibu hivi: ‘“Ninyi watu ndio mzigo! Nami nitawatupa,”+ asema Yehova.’ 34 Naye nabii au kuhani au mtu anayesema, ‘Huu ndio mzigo* wa Yehova!’ Nitamkazia fikira mtu huyo na nyumba yake. 35 Hivi ndivyo kila mmoja wenu anavyomwambia mwenzake na pia ndugu yake, ‘Yehova ametoa jibu gani? Na Yehova amesema nini?’ 36 Lakini msiutaje tena mzigo* wa Yehova, kwa maana mzigo* ni neno la kila mtu binafsi, nanyi mmeyabadili maneno ya Mungu aliye hai, Yehova wa majeshi, Mungu wetu.

37 “Utamuuliza nabii huyo hivi: ‘Yehova amekupa jibu gani? Na Yehova amesema nini? 38 Nanyi mkiendelea kusema, “Mzigo* wa Yehova!” Yehova anasema hivi: “Kwa sababu mnasema, ‘Hili neno ndilo mzigo* wa Yehova,’ baada ya mimi kuwaambia, ‘Msiseme: “Mzigo* wa Yehova!”’ 39 tazameni! Nitawainua juu na kuwatupa kutoka mbele zangu, ninyi pamoja na jiji nililowapa ninyi na mababu zenu. 40 Nami nitawaletea aibu ya milele na fedheha ya milele, ambayo haitasahauliwa.”’”+

24 Kisha Yehova akanionyesha vikapu viwili vya tini vilivyowekwa mbele ya hekalu la Yehova, baada ya Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni kumpeleka uhamishoni Yekonia*+ mwana wa Yehoyakimu,+ mfalme wa Yuda, pamoja na wakuu wa Yuda, mafundi, na wahunzi;* aliwatoa Yerusalemu na kuwapeleka Babiloni.+ 2 Kikapu kimoja kilikuwa na tini nzuri sana, kama tini za mapema, lakini kile kikapu kingine kilikuwa na tini mbaya sana, zilikuwa mbaya sana hivi kwamba hazingeweza kuliwa.

3 Kisha Yehova akaniuliza: “Unaona nini, Yeremia?” Basi nikasema: “Tini; tini nzuri ni nzuri sana, na tini mbaya ni mbaya sana, hivi kwamba haziwezi kuliwa.”+

4 Ndipo neno la Yehova likanijia likisema: 5 “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Kama hizi tini nzuri, ndivyo nitakavyowaona kwa njia nzuri wale watu wa Yuda waliohamishwa, ambao nimewatoa mahali hapa na kuwapeleka katika nchi ya Wakaldayo. 6 Jicho langu litaendelea kuwatazama kwa faida yao, nami nitawarudisha katika nchi hii.+ Nitawajenga, nami sitawabomoa; nitawapanda, nami sitawang’oa.+ 7 Nami nitawapa moyo wa kunijua, kwamba mimi ni Yehova.+ Watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao,+ kwa maana watarudi kwangu kwa moyo wao wote.+

8 “‘Lakini kuhusu tini mbaya ambazo ni mbaya sana hivi kwamba haziwezi kuliwa,+ Yehova anasema hivi: “Ndivyo nitakavyomwona Mfalme Sedekia+ wa Yuda, wakuu wake, wakaaji wa Yerusalemu waliobaki katika nchi hii, na wale wanaokaa nchini Misri.+ 9 Nitawafanya wawe kitu cha kutisha na msiba kwa falme zote za dunia,+ shutuma, methali, kitu cha kudhihakiwa, na laana+ kila mahali nitakapowatawanya.+ 10 Nami nitawaletea upanga,+ njaa kali, na ugonjwa hatari,+ mpaka waangamie kutoka katika nchi niliyowapa wao na mababu zao.”’”

25 Neno lililomjia Yeremia kuhusu watu wote wa Yuda katika mwaka wa nne wa utawala wa Yehoyakimu+ mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, ambao ulikuwa mwaka wa kwanza wa Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni. 2 Nabii Yeremia alisema hivi kuhusu* watu wote wa Yuda na wakaaji wote wa Yerusalemu:

3 “Tangu mwaka wa 13 wa utawala wa Yosia+ mwana wa Amoni, mfalme wa Yuda, mpaka leo hii, miaka hii 23, neno la Yehova limenijia, nami niliendelea kuwaambia tena na tena,* lakini hamkusikiliza.+ 4 Na Yehova aliwatuma kwenu watumishi wake wote manabii, aliwatuma tena na tena,* lakini hamkusikiliza, wala kutega sikio lenu ili msikie.+ 5 Walikuwa wakisema, ‘Tafadhali, geukeni kila mmoja wenu kutoka katika njia zenu za uovu na matendo yenu maovu;+ nanyi mtaendelea kukaa kwa muda mrefu katika nchi ambayo Yehova aliwapa ninyi na mababu zenu zamani. 6 Msiifuate miungu mingine na kuiabudu na kuiinamia, na kunikasirisha kwa kazi ya mikono yenu; la sivyo nitawaletea msiba.’

7 “‘Lakini hamkunisikiliza,’ asema Yehova, ‘Badala yake mlinikasirisha kwa kazi ya mikono yenu, na kujiletea msiba.’+

8 “Kwa hiyo Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘“Kwa sababu hamkuyatii maneno yangu, 9 ninaziita familia zote za kaskazini,”+ asema Yehova, “ninamwita Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni, mtumishi wangu,+ nami nitawaleta dhidi ya nchi hii+ na dhidi ya wakaaji wake na dhidi ya mataifa haya yote yanayozunguka.+ Nitawaangamiza na kuwafanya kuwa kitu cha kutisha na kitu cha kupigiwa mluzi na magofu ya kudumu. 10 Nitakomesha sauti ya furaha na sauti ya shangwe ndani yao,+ sauti ya bwana harusi na sauti ya bibi harusi,+ sauti ya jiwe la kusagia na nuru ya taa. 11 Na nchi hii yote itakuwa magofu na kitu cha kutisha, na mataifa haya yatalazimika kumtumikia mfalme wa Babiloni kwa miaka 70.”’+

12 “‘Lakini miaka 70 itakapotimia,+ nitamfanya mfalme wa Babiloni awajibike* na pia taifa hilo kwa sababu ya kosa lao,’+ asema Yehova, ‘nami nitaifanya nchi ya Wakaldayo kuwa mahame na ukiwa daima.+ 13 Nitatimiza maneno yangu yote niliyosema dhidi ya nchi hiyo, yote yaliyoandikwa katika kitabu hiki ambayo Yeremia ametabiri dhidi ya mataifa yote. 14 Kwa maana mataifa mengi na wafalme wakuu+ watawafanya kuwa watumwa,+ nami nitawalipa kulingana na matendo yao na kazi ya mikono yao wenyewe.’”+

15 Kwa maana Yehova Mungu wa Israeli aliniambia hivi: “Chukua kikombe hiki cha divai ya ghadhabu kutoka mkononi mwangu, nawe uyanyweshe mataifa yote ambayo ninakutuma kwao. 16 Nao watakunywa na kupepesuka na kutenda kama wendawazimu kwa sababu ya upanga ninaotuma miongoni mwao.”+

17 Basi nikakichukua kile kikombe kutoka mkononi mwa Yehova na kuyanywesha mataifa yote ambayo Yehova alinituma kwao:+ 18 kuanzia Yerusalemu na majiji ya Yuda,+ wafalme wake na wakuu wake, ili kuyafanya kuwa magofu, kitu cha kutisha, kitu cha kupigiwa mluzi na laana,+ kama ilivyo leo; 19 kisha mfalme Farao wa Misri na watumishi wake, wakuu wake, na watu wake wote,+ 20 na watu wa mataifa mbalimbali waliochangamana nao; wafalme wote wa nchi ya Usi; wafalme wote wa nchi ya Wafilisti,+ Ashkeloni,+ Gaza, Ekroni, na watu waliobaki wa Ashdodi; 21 Edomu,+ Moabu,+ na Waamoni;+ 22 wafalme wote wa Tiro, wafalme wote wa Sidoni,+ na wafalme wa kisiwa kilicho baharini; 23 Dedani,+ Tema, Buzi, na wale wote wanaonyoa nywele pembeni mwa vichwa vyao;+ 24 wafalme wote wa Waarabu+ na wafalme wote wa watu wa mataifa mbalimbali wanaokaa nyikani; 25 wafalme wote wa Zimri, wafalme wote wa Elamu,+ na wafalme wote wa Wamedi;+ 26 na wafalme wote wa kaskazini walio karibu na walio mbali, mmoja baada ya mwingine, na falme nyingine zote za dunia zilizo juu ya ardhi; na mfalme wa Sheshaki*+ atakunywa baada yao.

27 “Nawe unapaswa kuwaambia, ‘Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Kunyweni, mlewe, mtapike na kuanguka hivi kwamba msiweze kusimama+ kwa sababu ya upanga ninaotuma miongoni mwenu.”’ 28 Nao wakikataa kukichukua kikombe kutoka mkononi mwako ili wanywe, waambie, ‘Yehova wa majeshi anasema hivi: “Lazima mnywe! 29 Kwa maana tazama! ikiwa ninaleta msiba kwanza juu ya jiji linaloitwa kwa jina langu,+ je, ninyi pia hampaswi kuadhibiwa?”’+

“‘Hamtakosa kuadhibiwa, kwa maana ninauita upanga dhidi ya wakaaji wote wa dunia,’ asema Yehova wa majeshi.

30 “Nawe unapaswa kuwatabiria maneno haya yote, uwaambie,

‘Yehova atanguruma kutoka juu,

Kutoka katika makao yake matakatifu atafanya sauti yake isikike.

Atanguruma kwa sauti kubwa dhidi ya makao yake yanayodumu.

Atapaza sauti kama watu wanaokanyaga shinikizo la divai,

Ataimba kwa ushindi dhidi ya wakaaji wote wa dunia.’

31 ‘Kelele zitasikika mpaka kwenye miisho ya dunia,

Kwa maana Yehova ana kesi dhidi ya mataifa.

Yeye binafsi atawahukumu wanadamu wote.*+

Naye atawaangamiza waovu kwa upanga,’ asema Yehova.

32 Yehova wa majeshi anasema hivi:

‘Tazameni! Msiba unaenea kutoka taifa mpaka taifa,+

Na tufani kubwa itaachiliwa kutoka sehemu za mbali zaidi za dunia.+

33 “‘Na wale ambao Yehova atawaua siku hiyo watatapakaa kutoka mwisho mmoja wa dunia mpaka mwisho wa pili wa dunia. Hawataombolezewa, wala kukusanywa wala kuzikwa. Watakuwa kama mbolea juu ya ardhi.’

34 “Ombolezeni, enyi wachungaji, na mlie kwa sauti!

Mgaegae, enyi watu mashuhuri wa kundi,

Kwa sababu wakati wenu wa kuchinjwa na kutawanywa umefika,

Nanyi mtaanguka kama chombo chenye thamani!

35 Wachungaji hawana mahali pa kukimbilia,

Na watu mashuhuri wa kundi hawawezi kuponyoka.

36 Sikilizeni! Kilio cha wachungaji

Na kuomboleza kwa watu mashuhuri wa kundi,

Kwa maana Yehova anaharibu malisho yao.

37 Na makao yenye amani yamefanywa yasiwe na uhai

Kwa sababu ya hasira ya Yehova inayowaka.

38 Ametoka katika pango

lake kama mwanasimba,*+

Kwa maana nchi yao imekuwa kitu cha kutisha

Kwa sababu ya upanga wenye ukatili

Na kwa sababu ya hasira yake inayowaka.”

26 Mwanzoni mwa utawala wa Yehoyakimu+ mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, neno hili lilikuja kutoka kwa Yehova: 2 “Yehova anasema hivi: ‘Simama katika ua wa nyumba ya Yehova useme kuhusu* watu wote wa majiji ya Yuda wanaoingia ili kuabudu* katika nyumba ya Yehova. Waambie kila kitu ninachokuamuru; usiondoe hata neno moja. 3 Labda watasikiliza na kila mmoja ataiacha njia yake ovu, nami nitabadili nia yangu* kuhusu msiba ninaokusudia kuwaletea kwa sababu ya matendo yao maovu.+ 4 Waambie, “Yehova anasema hivi: ‘Ikiwa hamtanisikiliza kwa kufuata sheria* yangu niliyoweka mbele yenu, 5 kwa kuyasikiliza maneno ya watumishi wangu manabii, ninaowatuma kwenu tena na tena,* ambao hamjawasikiliza,+ 6 basi nitaifanya nyumba hii kama Shilo,+ nami nitalifanya jiji hili kuwa kitu cha kulaaniwa na mataifa yote ya dunia.’”’”+

7 Na makuhani na manabii na watu wote wakamsikia Yeremia akisema maneno hayo ndani ya nyumba ya Yehova.+ 8 Yeremia alipomaliza kusema mambo yote ambayo Yehova alimwamuru awaambie watu wote, ndipo makuhani na manabii na watu wote wakamkamata na kusema: “Hakika utakufa. 9 Kwa nini umetabiri katika jina la Yehova, ukisema, ‘Nyumba hii itakuwa kama Shilo, na jiji hili litaangamizwa na kuachwa bila mkaaji’?” Na watu wote wakakusanyika kumzunguka Yeremia ndani ya nyumba ya Yehova.

10 Wakuu wa Yuda waliposikia maneno hayo, wakapanda kutoka katika nyumba ya* mfalme wakaenda katika nyumba ya Yehova na kuketi kwenye njia inayoelekea kwenye lango jipya la Yehova.+ 11 Makuhani na manabii wakawaambia hivi wakuu na watu wote: “Mtu huyu anastahili hukumu ya kifo,+ kwa sababu ametabiri dhidi ya jiji hili kama mlivyosikia kwa masikio yenu wenyewe.”+

12 Ndipo Yeremia akawaambia wakuu wote na watu wote: “Yehova ndiye aliyenituma kutabiri dhidi ya nyumba hii na dhidi ya jiji hili maneno yote ambayo mmeyasikia.+ 13 Basi sasa rekebisheni njia zenu na matendo yenu nanyi mtii sauti ya Yehova Mungu wenu, naye Yehova atabadili nia yake* kuhusu msiba aliotangaza dhidi yenu.+ 14 Lakini mimi niko mikononi mwenu. Nitendeeni jambo lolote mnaloona kuwa jema na sawa machoni penu. 15 Ila tu mjue kwa hakika kwamba mkiniua, mtajiletea damu isiyo na hatia juu yenu na juu ya jiji hili na juu ya wakaaji wake, kwa maana kwa kweli Yehova alinituma kwenu ili niseme maneno haya mkiyasikia.”

16 Ndipo wakuu na watu wote wakawaambia makuhani na manabii: “Mtu huyu hastahili hukumu ya kifo, kwa maana alizungumza nasi katika jina la Yehova Mungu wetu.”

17 Zaidi ya hayo, baadhi ya wazee wa nchi wakasimama na kuanza kuliambia hivi kutaniko lote la watu: 18 “Mika+ wa Moreshethi alikuwa akitabiri katika siku za utawala wa Mfalme Hezekia+ wa Yuda, akawaambia watu wote wa Yuda, ‘Yehova wa majeshi anasema hivi:

“Sayuni litalimwa kama shamba,

Yerusalemu litakuwa marundo ya magofu,+

Na mlima wa Nyumba* utakuwa kama vilima msituni.”’*+

19 “Je, Mfalme Hezekia wa Yuda na watu wote wa Yuda walimuua? Je, hakumwogopa Yehova na kumwomba Yehova kibali,* hivi kwamba Yehova akabadili nia yake* kuhusu msiba aliotangaza dhidi yao?+ Basi tuko karibu kujiletea msiba mkubwa.

20 “Na kulikuwa na mtu mwingine aliyetabiri katika jina la Yehova, Uriya mwana wa Shemaya kutoka Kiriath-yearimu,+ aliyetabiri dhidi ya jiji hili na dhidi ya nchi hii kwa maneno kama ya Yeremia. 21 Mfalme Yehoyakimu+ na wanaume wake wote hodari na wakuu wote wakayasikia maneno yake, na mfalme alitaka kumuua.+ Uriya aliposikia jambo hilo, mara moja akaogopa na kukimbilia Misri. 22 Kisha Mfalme Yehoyakimu akamtuma Elnathani+ mwana wa Akbori pamoja na watu wengine kwenda Misri. 23 Wakamchukua Uriya kutoka Misri na kumpeleka kwa Mfalme Yehoyakimu, naye akamuua kwa upanga+ na kuitupa maiti yake katika makaburi ya watu wa kawaida.”

24 Lakini Ahikamu+ mwana wa Shafani+ alimsaidia Yeremia, ili asitiwe mikononi mwa watu na kuuawa.+

27 Mwanzoni mwa utawala wa Yehoyakimu mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, neno hili lilimjia Yeremia kutoka kwa Yehova: 2 “Yehova ameniambia hivi: ‘Jitengenezee mikanda na nira, nawe uziweke kwenye shingo yako. 3 Kisha upeleke vitu hivyo kwa mfalme wa Edomu,+ mfalme wa Moabu,+ mfalme wa Waamoni,+ mfalme wa Tiro,+ na kwa mfalme wa Sidoni+ kwa mkono wa wajumbe waliokuja Yerusalemu kwa Mfalme Sedekia wa Yuda. 4 Uwape amri hii kwa ajili ya mabwana wao:

“‘“Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema; waambieni hivi mabwana wenu: 5 ‘Mimi ndiye niliyeiumba dunia, wanadamu, na wanyama walio duniani kwa nguvu zangu kuu na kwa mkono wangu ulionyooshwa; nami nimempa yeyote ninayetaka.*+ 6 Na sasa mimi mwenyewe nimezitia nchi hizi zote mikononi mwa mtumishi wangu Mfalme Nebukadneza+ wa Babiloni; nimempa hata wanyama wa mwituni ili wamtumikie. 7 Mataifa yote yatamtumikia yeye na mwanawe na mjukuu wake mpaka wakati wa nchi yake utakapofika,+ wakati ambapo mataifa mengi na wafalme wakuu watamfanya kuwa mtumwa wao.’+

8 “‘“‘Ikiwa taifa lolote au ufalme utakataa kumtumikia Mfalme Nebukadneza wa Babiloni na kukataa kuweka shingo yake chini ya nira ya mfalme wa Babiloni, nitaliadhibu taifa hilo kwa upanga,+ kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari,’ asema Yehova, ‘mpaka nitakapowaangamiza kwa mkono wake.’

9 “‘“‘Kwa hiyo, msiwasikilize manabii wenu, waaguzi* wenu, waota-ndoto wenu, wachawi wenu, na walozi wenu, wanaowaambia: “Hamtamtumikia mfalme wa Babiloni.” 10 Kwa maana wanawatabiria uwongo, ili mpelekwe mbali na nchi yenu, nami nitawatawanya ninyi, nanyi mtaangamia.

11 “‘“‘Lakini taifa litakaloweka shingo yake chini ya nira ya mfalme wa Babiloni na kumtumikia, nitaliruhusu libaki* kwenye nchi yake,’ asema Yehova, ‘ili kuilima na kukaa ndani yake.’”’”

12 Pia nilimwambia Mfalme Sedekia+ wa Yuda maneno hayohayo, nikisema: “Wekeni shingo zenu chini ya nira ya mfalme wa Babiloni na mumtumikie yeye na watu wake, nanyi mtaendelea kuishi.+ 13 Kwa nini wewe na watu wako mfe kwa upanga,+ kwa njaa kali,+ na kwa ugonjwa hatari,+ kama Yehova alivyosema kuhusu taifa ambalo halitamtumikia mfalme wa Babiloni? 14 Msiyasikilize maneno ya manabii wanaowaambia, ‘Hamtamtumikia mfalme wa Babiloni,’+ kwa sababu wanawatabiria uwongo.+

15 “‘Kwa maana sijawatuma,’ asema Yehova, ‘lakini wanatabiri uwongo katika jina langu, ili mwishowe niwatawanye na mwangamie, ninyi na manabii wanaowatabiria ninyi.’”+

16 Nami nikawaambia makuhani na watu hawa wote, “Yehova anasema hivi: ‘Msiyasikilize maneno ya manabii wenu wanaowatabiria wakisema: “Tazameni! Vyombo vya nyumba ya Yehova vitarudishwa kutoka Babiloni hivi karibuni!”+ kwa maana wanawatabiria uwongo.+ 17 Msiwasikilize. Mtumikieni mfalme wa Babiloni nanyi mtaendelea kuishi.+ Kwa nini jiji hili liwe magofu? 18 Lakini ikiwa wao ni manabii na ikiwa wana neno la Yehova, tafadhali acheni wamwombe Yehova wa majeshi kwamba vyombo vilivyobaki katika nyumba ya Yehova, katika nyumba ya* mfalme wa Yuda, na Yerusalemu visipelekwe Babiloni.’

19 “Kwa maana Yehova wa majeshi anasema hivi kuhusu zile nguzo,+ ile Bahari,*+ yale magari,+ na vyombo vilivyobaki vilivyoachwa katika jiji hili, 20 ambavyo Mfalme Nebukadneza wa Babiloni hakuvichukua alipompeleka uhamishoni Yekonia mwana wa Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, kutoka Yerusalemu hadi Babiloni, pamoja na watu wote wenye vyeo wa Yuda na Yerusalemu;+ 21 naam, Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli anasema hivi kuhusu vyombo vilivyobaki katika nyumba ya Yehova, katika nyumba ya* mfalme wa Yuda, na Yerusalemu: 22 ‘“Vitapelekwa Babiloni,+ navyo vitabaki huko mpaka siku nitakapovikazia fikira,” asema Yehova. “Kisha nitavileta na kuvirudisha mahali hapa.”’”+

28 Mwaka huohuo, mwanzoni mwa utawala wa Mfalme Sedekia+ wa Yuda, katika mwaka wa nne, mwezi wa tano, nabii Hanania mwana wa Azuri kutoka Gibeoni+ aliniambia hivi katika nyumba ya Yehova mbele ya makuhani na watu wote: 2 “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi, ‘Nitaivunja nira ya mfalme wa Babiloni.+ 3 Katika muda wa miaka miwili* nitavirudisha mahali hapa vyombo vyote vya nyumba ya Yehova ambavyo Mfalme Nebukadneza wa Babiloni alivichukua mahali hapa na kuvipeleka Babiloni.’”+ 4 “‘Nami nitamrudisha mahali hapa Yekonia+ mwana wa Yehoyakimu,+ mfalme wa Yuda, na watu wote wa Yuda waliohamishwa na kupelekwa Babiloni,’+ asema Yehova, ‘kwa maana nitaivunja nira ya mfalme wa Babiloni.’”

5 Kisha nabii Yeremia akazungumza na nabii Hanania mbele ya makuhani na watu wote waliokuwa wamesimama katika nyumba ya Yehova. 6 Nabii Yeremia akasema: “Amina!* Yehova na afanye hivyo! Yehova na atimize maneno yako uliyotabiri kwa kuvirudisha mahali hapa vyombo vya nyumba ya Yehova kutoka Babiloni na pia watu wote waliopelekwa uhamishoni! 7 Hata hivyo, tafadhali sikia ujumbe huu ninaosema masikioni mwako na masikioni mwa watu wote. 8 Zamani za kale manabii walionitangulia mimi na waliokutangulia wewe walikuwa wakitabiri kuhusu nchi nyingi na falme kubwa, kuhusu vita, misiba, na magonjwa hatari. 9 Nabii akitabiri amani na neno la nabii huyo litimie, basi itajulikana kwamba kwa kweli Yehova amemtuma nabii huyo.”

10 Ndipo nabii Hanania akaichukua ile nira kutoka shingoni mwa nabii Yeremia na kuivunja.+ 11 Kisha Hanania akasema mbele ya watu wote: “Yehova anasema hivi: ‘Hivyo ndivyo nitakavyoivunja nira ya Mfalme Nebukadneza wa Babiloni kutoka shingoni mwa mataifa yote katika muda wa miaka miwili.’”+ Kisha nabii Yeremia akaenda zake.

12 Baada ya nabii Hanania kuivunja ile nira kutoka shingoni mwa nabii Yeremia, ujumbe huu wa Yehova ukamjia Yeremia: 13 “Nenda umwambie Hanania, ‘Yehova anasema hivi: “Umevunja nira za mbao,+ lakini badala yake utatengeneza nira za chuma.” 14 Kwa maana Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Nitaweka nira ya chuma juu ya shingo ya mataifa haya yote, ili yamtumikie Mfalme Nebukadneza wa Babiloni, nayo lazima yamtumikie.+ Nitampa hata wanyama wa mwituni.”’”+

15 Kisha nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania:+ “Tafadhali, sikiliza, ewe Hanania! Yehova hakukutuma wewe, bali umewafanya watu hawa wautumaini uwongo.+ 16 Kwa hiyo Yehova anasema hivi: ‘Tazama! Ninakuondoa katika uso wa nchi. Utakufa mwaka huu, kwa maana umewachochea watu wamwasi Yehova.’”+

17 Basi nabii Hanania akafa mwaka huo, katika mwezi wa saba.

29 Haya ndiyo maneno ya barua ambayo nabii Yeremia aliwatumia kutoka Yerusalemu wazee waliobaki miongoni mwa watu waliopelekwa uhamishoni, makuhani, manabii, na watu wote, ambao Nebukadneza alikuwa amewatoa Yerusalemu na kuwapeleka uhamishoni Babiloni, 2 baada ya Mfalme Yekonia+ na mama malkia,+ maofisa wa makao ya mfalme, wakuu wa Yuda na Yerusalemu, na mafundi na wahunzi* kuondoka Yerusalemu.+ 3 Aliituma barua hiyo kwa mkono wa Elasa mwana wa Shafani+ na Gemaria mwana wa Hilkia, ambao Mfalme Sedekia+ wa Yuda aliwatuma kwenda Babiloni kwa Mfalme Nebukadneza wa Babiloni. Barua hiyo ilisema hivi:

4 “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anawaambia hivi watu wote waliohamishwa, ambao aliwafanya wapelekwe uhamishoni Babiloni kutoka Yerusalemu, 5 ‘Jengeni nyumba mkae ndani yake. Pandeni bustani na mle matunda yake. 6 Oeni wake mzae wana na mabinti; wachukulieni wana wenu wake na kuwaoza mabinti wenu, ili wao pia wazae wana na mabinti. Muwe wengi huko, msipungue. 7 Nanyi tafuteni amani kwa ajili ya jiji ambamo nimewapeleka uhamishoni, nanyi msali kwa Yehova kwa ajili ya jiji hilo, kwa maana jiji hilo likiwa na amani mtakuwa na amani.+ 8 Kwa maana Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Msiwaruhusu manabii wenu na waaguzi* wenu walio miongoni mwenu wawadanganye,+ nanyi msisikilize ndoto wanazoota. 9 Kwa maana ‘wanawatabiria uwongo katika jina langu. Mimi sijawatuma,’+ asema Yehova.”’”

10 “Kwa maana Yehova anasema hivi: ‘Miaka 70 itakapotimia huko Babiloni nitawakazia ninyi fikira,+ nami nitatimiza ahadi yangu kwa kuwarudisha mahali hapa.’+

11 “‘Kwa maana ninajua vizuri mawazo ninayofikiria kuwaelekea ninyi,’ asema Yehova, ‘mawazo ya amani, wala si ya msiba,+ ili niwape ninyi wakati ujao na tumaini.+ 12 Nanyi mtaniita na kuja na kusali kwangu, nami nitawasikiliza.’+

13 “‘Mtanitafuta na kunipata,+ kwa maana mtanitafuta kwa moyo wenu wote.+ 14 Nami nitawaruhusu mnipate,’+ asema Yehova. ‘Nami nitawakusanya mateka wenu na kuwakusanya ninyi pamoja kutoka katika mataifa yote na sehemu zote nilizowatawanya,’+ asema Yehova. ‘Nami nitawarudisha mahali nilipowatoa nikawapeleka uhamishoni.’+

15 “Lakini ninyi mmesema, ‘Yehova ametuinulia manabii katika Babiloni.’

16 “Kwa maana Yehova anamwambia hivi mfalme anayeketi kwenye kiti cha ufalme cha Daudi+ na watu wote wanaokaa katika jiji hili, ndugu zenu ambao hawakwenda pamoja nanyi uhamishoni, 17 ‘Yehova wa majeshi anasema hivi: “Tazameni, ninatuma dhidi yao upanga, njaa kali, na ugonjwa hatari,+ nami nitawafanya kuwa kama tini zilizooza* ambazo ni mbaya sana hivi kwamba haziwezi kuliwa.”’+

18 “‘Nami nitawafuatia kwa upanga,+ kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari, nami nitawafanya wawe kitu cha kutisha kwa falme zote za dunia,+ na laana, na kitu cha kushangaza, kitu cha kupigiwa mluzi,+ na shutuma miongoni mwa mataifa yote ambako nitawatawanya,+ 19 kwa sababu hawakuyasikiliza maneno yangu niliyowapa kupitia watumishi wangu manabii,’ asema Yehova, ‘ambao niliwatuma tena na tena.’*+

“‘Lakini hamkusikiliza,’+ asema Yehova.

20 “Kwa hiyo, sikieni neno la Yehova, ninyi nyote mliopelekwa uhamishoni, niliowatoa Yerusalemu na kuwapeleka Babiloni. 21 Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi kuhusu Ahabu mwana wa Kolaya na kuhusu Sedekia mwana wa Maaseya, wanaowatabiria uwongo katika jina langu:+ ‘Nitawatia mikononi mwa Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni, naye atawaua mbele ya macho yenu. 22 Na kile kitakachowapata kitakuwa laana itakayosemwa na watu wote wa Yuda walio uhamishoni Babiloni: “Yehova na akutendee kama Sedekia na kama Ahabu, ambao mfalme wa Babiloni aliwateketeza motoni!” 23 kwa maana wametenda kwa aibu katika Israeli,+ wakifanya uzinzi na wake za majirani wao na kusema maneno ya uwongo katika jina langu, maneno ambayo sikuwaamuru.+

“‘“Mimi Ndiye ninayejua, nami ni shahidi,”+ asema Yehova.’”

24 “Nawe utamwambia hivi Shemaya+ wa Nehelamu: 25 ‘Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Kwa sababu ulituma barua katika jina lako kwa watu wote walio Yerusalemu, kwa Sefania+ mwana wa Maaseya, kuhani, na kwa makuhani wote, ukisema, 26 ‘Yehova amekuweka kuwa kuhani badala ya kuhani Yehoyada, ili uwe mwangalizi wa nyumba ya Yehova, uwe msimamizi wa mwendawazimu yeyote anayetenda kama nabii na kumweka katika mikatale na katika kongwa;*+ 27 basi, kwa nini hujamkemea Yeremia wa Anathothi,+ anayetenda kama nabii wenu?+ 28 Kwa maana hata alitutumia ujumbe Babiloni, akisema: “Muda mrefu utapita! Jengeni nyumba na mkae ndani yake. Pandeni bustani na mle matunda yake,+—”’”’”

29 Kuhani Sefania+ alipoisoma barua hiyo mbele ya nabii Yeremia, 30 Neno la Yehova likamjia Yeremia likisema: 31 “Watumie ujumbe watu wote waliopelekwa uhamishoni, ukisema, ‘Yehova anasema hivi kumhusu Shemaya wa Nehelamu: “Kwa sababu Shemaya aliwatabiria, ingawa sikumtuma, naye akajaribu kuwafanya mtumaini uwongo,+ 32 kwa hiyo Yehova anasema hivi: ‘Ninamkazia fikira Shemaya wa Nehelamu na wazao wake. Hakuna yeyote miongoni mwa watu wake atakayeokoka kati ya watu hawa, naye hataona mema nitakayowatendea watu wangu,’ asema Yehova, ‘kwa maana amewachochea watu wamwasi Yehova.’”’”

30 Neno hili lilimjia Yeremia kutoka kwa Yehova, likisema: 2 “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Andika katika kitabu maneno yote ninayokuambia. 3 Kwa maana “tazama! siku zinakuja,” asema Yehova, “nitakapowakusanya watu wangu waliotekwa, Israeli na Yuda,”+ asema Yehova, “nami nitawarudisha katika nchi niliyowapa mababu zao, nao wataimiliki tena.”’”+

4 Haya ndiyo maneno ambayo Yehova aliwaambia watu wa Israeli na Yuda.

 5 Yehova anasema hivi:

“Tumesikia sauti za kutetemeka;

Kuna hofu, na hakuna amani.

 6 Ulizeni, tafadhali, ikiwa mwanamume anaweza kujifungua mtoto.

Hivyo basi, kwa nini ninamwona kila mwanamume mwenye nguvu akishika tumbo lake*

Kama mwanamke anayejifungua?+

Kwa nini kila uso umegeuka rangi?

 7 Ole wangu! Kwa maana siku hiyo inatisha sana.*+

Hakuna nyingine kama hiyo,

Wakati wa taabu kwa Yakobo.

Lakini ataokolewa kutokana nayo.”

8 “Na siku hiyo,” asema Yehova wa majeshi, “nitaivunja nira kutoka shingoni mwako, na mikanda yako nitaikata* vipande viwili; na wageni* hawatamfanya* tena kuwa mtumwa wao. 9 Watamtumikia Yehova Mungu wao na Daudi mfalme wao, ambaye nitamweka juu yao.”+

10 “Nawe, mtumishi wangu Yakobo, usiogope,” asema Yehova,

“Wala usihofu, Ee Israeli.+

Kwa maana nitakuokoa kutoka mbali

Na uzao wako kutoka katika nchi waliyopelekwa utekwani.+

Yakobo atarudi na kuwa na utulivu bila usumbufu,

Na hakuna yeyote atakayewaogopesha.”+

11 “Kwa maana mimi niko pamoja nawe,” asema Yehova, “ili nikuokoe.

Lakini nitaleta maangamizi katika mataifa yote ambako nilikutawanya;+

Lakini wewe, sitakuangamiza.+

Nitakutia nidhamu* kwa kiwango kinachofaa,

Nami sitakuacha kamwe bila kukuadhibu.”+

12 Kwa maana Yehova anasema hivi:

“Hakuna matibabu kwa ajili ya jeraha lako.*+

Kidonda chako hakiwezi kupona.

13 Hakuna mtu wa kukutetea,

Hakuna njia ya kukiponya kidonda chako.

Hakuna dawa ya kukuponya.

14 Wapenzi wako wote wamekusahau.+

Hawakutafuti tena.

Kwa maana nimekupiga kwa pigo la adui,+

Kwa adhabu ya mtu mkatili,

Kwa sababu ya hatia yako kubwa na dhambi zako nyingi.+

15 Kwa nini unapaza kilio kwa sababu ya jeraha lako?*

Maumivu yako hayawezi kupona!

Kwa sababu ya hatia yako kubwa na dhambi zako nyingi+

Nimekutendea hivyo.

16 Kwa hiyo wale wote wanaokumeza, watamezwa,+

Na maadui wako wote watapelekwa pia utekwani.+

Wale wanaokupora wataporwa,

Nami nitawatia mikononi mwa waporaji wale wote wanaokupora.”+

17 “Lakini nitakurudishia afya yako na kuyaponya majeraha yako,”+ asema Yehova,

“Ingawa walikuita mtu aliyetengwa:

‘Sayuni, asiyetafutwa na yeyote.’”+

18 Yehova anasema hivi:

“Ninawakusanya mateka wa mahema ya Yakobo,+

Nami nitayahurumia makao yake.

Jiji litajengwa upya juu ya kilima chake,+

Na mnara wenye ngome utasimama mahali pake panapofaa.

19 Na kutoka kwao kutakuwa na shukrani na sauti za kicheko.+

Nitawazidisha, nao hawatakuwa wachache;+

Nitawafanya kuwa wengi,*

Nao hawatakuwa duni.+

20 Wanawe watakuwa kama walivyokuwa zamani,

Na kusanyiko lake litaimarishwa kabisa mbele zangu.+

Nitakabiliana na wote wanaomkandamiza.+

21 Mtu wake mashuhuri atatoka kati yake,

Na mtawala wake atatoka kati yake.

Nitamfanya akaribie, naye atanikaribia.”

“La sivyo, ni nani anayeweza kuthubutu kunikaribia?”* asema Yehova.

22 “Nanyi mtakuwa watu wangu,+ nami nitakuwa Mungu wenu.”+

23 Tazameni! Dhoruba ya Yehova ya upepo italipuka kwa ghadhabu,+

Tufani inayofagia ambayo inazunguka ikishuka juu ya kichwa cha waovu.

24 Hasira inayowaka ya Yehova haitapoa

Mpaka atakapotekeleza na kutimiza makusudi ya moyo wake.+

Mtaelewa jambo hilo katika siku za mwisho.+

31 “Wakati huo,” asema Yehova, “Nitakuwa Mungu wa familia zote za Israeli, nao watakuwa watu wangu.”+

 2 Yehova anasema hivi:

“Watu waliookoka upanga walipata kibali nyikani

Israeli alipokuwa akitembea kwenda mahali pake pa kupumzika.”

 3 Kutoka mbali Yehova alinitokea na kusema:

“Nimekupenda kwa upendo wa milele.

Ndiyo sababu nimekuvuta kwangu kwa upendo mshikamanifu.*+

 4 Kwa mara nyingine tena nitakujenga upya nawe utajengwa upya.+

Ewe bikira wa Israeli, utachukua tena matari yako

Na kwenda ukicheza dansi kwa shangwe.*+

 5 Utapanda tena mashamba ya mizabibu kwenye milima ya Samaria;+

Wanaopanda watapanda na kufurahia matunda yake.+

 6 Kwa maana siku itafika ambayo walinzi walio kwenye milima ya Efraimu watapaza sauti wakisema:

‘Inukeni, twendeni juu Sayuni, kwa Yehova Mungu wetu.’”+

 7 Kwa maana Yehova anasema hivi:

“Mlilieni Yakobo kwa shangwe.

Pigeni vigelegele vya shangwe kwa sababu mko juu ya mataifa.+

Tangazeni jambo hilo; sifuni na kusema,

‘Ee Yehova, waokoe watu wako, Waisraeli wanaobaki.’+

 8 Ninawarudisha kutoka nchi ya kaskazini.+

Nitawakusanya pamoja kutoka sehemu za mbali zaidi za dunia.+

Miongoni mwao kutakuwa na vipofu na vilema,+

Mwanamke mwenye mimba na yule anayezaa, wote pamoja.

Watarudi hapa wakiwa kutaniko kubwa.+

 9 Watakuja wakilia.+

Nitawaongoza huku wakiomba kibali.

Nitawaongoza kwenye vijito vya* maji,+

Kwenye kijia tambarare ambacho hakitawafanya wajikwae.

Kwa maana mimi ni Baba ya Israeli, naye Efraimu ni mzaliwa wangu wa kwanza.”+

10 Sikieni neno la Yehova, enyi mataifa,

Na mlitangaze kati ya visiwa vilivyo mbali sana:+

“Yule aliyemtawanya Israeli atamkusanya pamoja.

Atamlinda kama mchungaji anavyochunga kundi lake.+

11 Kwa maana Yehova atamkomboa Yakobo+

Na kumwokoa* kutoka mikononi mwa yule aliye na nguvu zaidi yake.+

12 Watakuja na kupiga vigelegele vya shangwe juu ya kilele cha Sayuni+

Na kung’aa kwa sababu ya wema wa* Yehova,

Kwa sababu ya nafaka na divai mpya+ na mafuta,

Na kwa sababu ya wanakondoo na ndama.+

Watakuwa* kama bustani iliyonyweshwa maji vizuri,+

Nao hawatadhoofika tena.”+

13 “Wakati huo bikira atacheza dansi kwa shangwe,

Pia wanaume vijana na wanaume wazee pamoja.+

Nitayageuza maombolezo yao yawe furaha.+

Nitawafariji na kuwafanya washangilie badala ya kuhuzunika.+

14 Nami nitawashibisha makuhani kwa vitu vingi,*

Na watu wangu watashiba wema wangu,”+ asema Yehova.

15 “Yehova anasema hivi:

‘Sauti inasikika kule Rama,+ maombolezo na kilio cha uchungu:

Raheli anawalilia wanawe.*+

Amekataa kufarijiwa kuhusiana na wanawe,

Kwa sababu hawako tena.’”+

16 Yehova anasema hivi:

“‘Zuia sauti yako usilie na macho yako yasitokwe na machozi,

Kwa maana utapata thawabu kwa ajili ya kazi yako,’ asema Yehova.

‘Watarudi kutoka nchi ya adui.’+

17 ‘Na kuna tumaini kwa ajili ya wakati wako ujao,’+ asema Yehova.

‘Wana wako watarudi kwenye eneo lao wenyewe.’”+

18 “Hakika nimemsikia Efraimu akiomboleza,

‘Umenirekebisha, nami nimerekebishwa,

Kama ndama ambaye hajazoezwa.

Nirudishe, nami nitageuka bila kusita,

Kwa maana wewe ni Yehova Mungu wangu.

19 Kwa maana baada ya kugeuka nilijuta;+

Baada ya kusaidiwa kuelewa nilipiga paja langu kwa huzuni.

Niliaibika na kufedheheka,+

Kwa maana nilibeba shutuma ya ujana wangu.’”

20 “Je, Efraimu si mwana mwenye thamani kwangu, au mtoto mpendwa?+

Kwa maana kila mara ninapomshutumu, bado ninamkumbuka.

Ndiyo sababu hisia zangu zimechochewa* kwa ajili yake.+

Nami hakika nitamhurumia,” asema Yehova.+

21 “Jiwekee alama za barabara,

Na uweke vibao vya ishara.+

Kazia fikira barabara kuu, njia ambayo unapaswa kupitia.+

Rudi, ewe bikira wa Israeli, rudi kwenye majiji haya yako.

22 Utaendelea kuyumbayumba mpaka lini, ewe binti usiye mwaminifu?

Kwa maana Yehova ameumba jambo jipya duniani:

Mwanamke atamtafuta mwanamume kwa bidii.”

23 Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Watasema tena maneno haya katika nchi ya Yuda na katika majiji yake nitakapowakusanya na kuwarudisha mateka wao: ‘Yehova na akubariki, Ee makao ya uadilifu,+ Ee mlima mtakatifu.’+ 24 Na watu wa Yuda na majiji yake yote watakaa pamoja ndani yake, wakulima na wale wanaochunga kondoo.+ 25 Kwa maana nitamshibisha aliyechoka na kumjaza kila mtu aliyedhoofika.”+

26 Ndipo nikaamka na kufungua macho yangu, na usingizi wangu ulikuwa mtamu.

27 “Tazama! Siku zinakuja,” asema Yehova, “nitakapoipanda nyumba ya Israeli na nyumba ya Yuda kwa mbegu ya* mwanadamu na kwa mbegu ya mifugo.”+

28 “Na kama nilivyowakazia uangalifu ili kuwang’oa, kuwabomoa, kuwaangusha, kuwaharibu, na kuwadhuru,+ ndivyo nitakavyowakazia uangalifu ili kuwajenga na kuwapanda,”+ asema Yehova. 29 “Katika siku hizo hawatasema tena, ‘Akina baba walikula zabibu chachu, lakini meno ya wana ndiyo yaliyotiwa ukakasi.’*+ 30 Lakini wakati huo kila mtu atakufa kwa sababu ya kosa lake mwenyewe. Mtu yeyote atakayekula zabibu chachu, atatiwa ukakasi kwenye meno yake mwenyewe.”

31 “Tazama! Siku zinakuja,” asema Yehova, “nitakapofanya agano jipya pamoja na nyumba ya Israeli na nyumba ya Yuda.+ 32 Halitakuwa kama agano nililofanya pamoja na mababu zao siku niliyowashika mkono na kuwaongoza kutoka nchini Misri,+ ‘agano langu ambalo walilivunja,+ ingawa nilikuwa bwana* wao wa kweli,’ asema Yehova.”

33 “Kwa maana hili ndilo agano nitakalofanya pamoja na nyumba ya Israeli baada ya siku hizo,” asema Yehova. “Nitaitia sheria yangu ndani yao,+ nami nitaiandika katika moyo wao.+ Nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.”+

34 “Nao hawatafundishana tena kila mtu na jirani yake na kila mtu na ndugu yake, wakisema, ‘Mjue Yehova!’+ kwa maana wote watanijua, kuanzia mdogo zaidi mpaka mkubwa zaidi kati yao,”+ asema Yehova. “Kwa maana nitalisamehe kosa lao, nami sitaikumbuka tena dhambi yao.”+

35 Yehova,

Ambaye hutoa jua ili liangaze wakati wa mchana,

Sheria za* mwezi na nyota ili ziangaze usiku,

Anayeitibua bahari na kuyavuruga mawimbi yake,

Ambaye jina lake ni Yehova wa majeshi, anasema hivi:+

36 “‘Ikiwa sheria hizo zitakoma,’ asema Yehova,

‘Basi uzao wa Israeli utakoma daima kuwa taifa mbele zangu.’”+

37 Yehova anasema hivi: “‘Ikiwa mbingu zilizo juu zinaweza kupimwa na misingi ya dunia iliyo chini kuchunguzwa, basi ninaweza kuukataa uzao wote wa Israeli kwa sababu ya yote ambayo wamefanya,’ asema Yehova.”+

38 “Tazama! Siku zinakuja,” asema Yehova, “ambapo jiji litajengwa+ kwa ajili ya Yehova kutoka Mnara wa Hananeli+ mpaka Lango la Pembeni.+ 39 Nayo kamba ya kupimia+ itaenda moja kwa moja mpaka kwenye kilima cha Garebu, nayo itageuka na kuelekea Goa. 40 Na bonde lote la mizoga na la* majivu,* na matuta yote mpaka Bonde la Kidroni,+ mpaka kwenye pembe ya Lango la Farasi+ kuelekea mashariki, litakuwa kitu kitakatifu kwa Yehova.+ Halitang’olewa tena kamwe wala kubomolewa.”

32 Neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Yehova katika mwaka wa 10 wa utawala wa Mfalme Sedekia wa Yuda, yaani, mwaka wa 18 wa utawala wa Nebukadneza.*+ 2 Wakati huo majeshi ya mfalme wa Babiloni yalikuwa yakizingira Yerusalemu, naye nabii Yeremia alikuwa amezuiliwa katika Ua wa Walinzi+ katika nyumba ya* mfalme wa Yuda. 3 Kwa maana Mfalme Sedekia wa Yuda alikuwa amemzuilia,+ akisema: “Kwa nini unatabiri hivi? Unasema, ‘Yehova anasema hivi: “Nitalitia jiji hili mikononi mwa mfalme wa Babiloni, naye ataliteka,+ 4 na Mfalme Sedekia wa Yuda hataponyoka kutoka kwa Wakaldayo, kwa maana hakika atatiwa mikononi mwa mfalme wa Babiloni, naye atazungumza naye uso kwa uso na kumwona jicho kwa jicho.”+ 5 ‘Atampeleka Sedekia Babiloni, naye atakaa huko mpaka nitakapomkazia fikira,’ asema Yehova. ‘Ingawa mnaendelea kupigana na Wakaldayo, hamtafanikiwa.’”+

6 Yeremia akasema: “Neno la Yehova limenijia likisema, 7 ‘Hanameli mwana wa Shalumu ndugu ya baba yako atakuja kwako na kukuambia: “Nunua shamba langu lililo Anathothi,+ kwa sababu una haki ya kwanza ya kulikomboa.”’”+

8 Hanameli mwana wa ndugu ya baba yangu akaja kwangu, kama Yehova alivyosema, katika Ua wa Walinzi, naye akaniambia: “Tafadhali nunua shamba langu lililo Anathothi, katika nchi ya Benjamini, kwa maana una haki ya kulimiliki na kulikomboa. Linunue liwe lako.” Ndipo nikajua kwamba hilo lilikuwa neno la Yehova.

9 Basi nikalinunua shamba lililokuwa Anathothi kutoka kwa Hanameli mwana wa ndugu ya baba yangu. Nikampimia pesa,+ shekeli saba* na vipande kumi vya fedha. 10 Kisha nikaandika katika hati,+ nikaitia muhuri, nikawaita mashahidi,+ nami nikapima pesa kwa mizani. 11 Nikaichukua ile hati ya ununuzi, iliyotiwa muhuri kulingana na amri na masharti ya kisheria, na pia hati ambayo haikuwa na muhuri, 12 kisha nikampa hati hiyo ya ununuzi Baruku+ mwana wa Neria+ mwana wa Mahseya mbele ya Hanameli mwana wa ndugu ya baba yangu, wale mashahidi walioandika kwenye hati ya ununuzi, na Wayahudi wote waliokuwa wameketi katika Ua wa Walinzi.+

13 Sasa nikamwamuru Baruku mbele yao, nikisema: 14 “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Chukua hati hizi, hati hii ya ununuzi, iliyotiwa muhuri na ile hati nyingine isiyo na muhuri, nawe uziweke katika chombo cha udongo, ili zihifadhiwe kwa muda mrefu.’ 15 Kwa maana Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Nyumba na mashamba na mashamba ya mizabibu yatanunuliwa tena katika nchi hii.’”+

16 Kisha nikasali kwa Yehova baada ya kumpa Baruku mwana wa Neria ile hati ya ununuzi, nikisema: 17 “Ole wangu, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Tazama! Uliumba mbingu na dunia kwa nguvu zako kuu+ na kwa mkono wako ulionyooshwa. Hakuna jambo la ajabu sana kwako, 18 Wewe unayewatendea kwa upendo mshikamanifu maelfu ya watu, lakini unawaadhibu wana kwa sababu ya makosa ya baba zao,+ Mungu wa kweli, uliye mkuu na Mwenye nguvu, ambaye jina lako ni Yehova wa majeshi. 19 Wewe ni mkuu katika kutoa mashauri* na matendo yako ni yenye nguvu,+ wewe ambaye macho yako huchunguza njia zote za wanadamu,+ ili kumlipa kila mtu kulingana na njia zake na matendo yake.+ 20 Umefanya ishara na miujiza katika nchi ya Misri, nayo inajulikana mpaka leo hii, na hivyo umejijengea jina katika Israeli na kati ya wanadamu,+ kama ilivyo leo. 21 Nawe uliwatoa watu wako Waisraeli nchini Misri, kwa ishara, kwa miujiza, kwa mkono wenye nguvu, kwa mkono ulionyooshwa, na kwa matendo yanayoogopesha.+

22 “Baada ya muda ukawapa nchi hii ambayo uliapa kwamba utawapa mababu zao,+ nchi inayotiririka maziwa na asali.+ 23 Nao wakaingia na kuimiliki, lakini hawakuitii sauti yako wala kutembea katika sheria yako. Hawakufanya lolote kati ya mambo uliyowaamuru wafanye, hivi kwamba ukawaletea msiba huu wote.+ 24 Tazama! Watu wamekuja na maboma ya kuzingira ili kuliteka jiji hili,+ na kwa sababu ya upanga,+ njaa kali, na ugonjwa hatari,+ hakika jiji litaanguka mikononi mwa Wakaldayo wanaolishambulia; mambo uliyosema yametimia yote, kama unavyoona sasa. 25 Lakini umeniambia, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘Nunua shamba kwa pesa na uwaite mashahidi,’ ingawa kwa hakika jiji litatiwa mikononi mwa Wakaldayo.”

26 Ndipo neno la Yehova likamjia Yeremia likisema: 27 “Mimi ndimi, Yehova, Mungu wa wanadamu wote.* Je, kuna jambo lolote ambalo ni la ajabu sana kwangu? 28 Basi Yehova anasema hivi: ‘Tazama, ninalitia jiji hili mikononi mwa Wakaldayo na mikononi mwa Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni, naye ataliteka.+ 29 Na Wakaldayo wanaolishambulia jiji hili wataingia na kulichoma moto jiji hili na kuliteketeza+ pamoja na nyumba ambazo juu ya paa zake watu walimtolea dhabihu Baali na kuitolea miungu mingine matoleo ya kinywaji ili kunikasirisha.’+

30 “‘Kwa maana watu wa Israeli na wa Yuda wametenda maovu tu machoni pangu, tangu ujana wao;+ watu wa Israeli wanaendelea kunikasirisha kwa kazi ya mikono yao,’ asema Yehova. 31 ‘Kwa maana jiji hili, tangu siku walipolijenga mpaka leo hii, limekuwa tu likinikasirisha na kunitia ghadhabu,+ hivi kwamba ni lazima liondolewe mbele za uso wangu,+ 32 kwa sababu ya uovu wote ambao watu wa Israeli na wa Yuda walifanya ili kunikasirisha—wao, wafalme wao,+ wakuu wao,+ makuhani wao, manabii wao,+ na watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu. 33 Waliendelea kunigeuzia migongo yao, si nyuso zao;+ ingawa nilijaribu kuwafundisha tena na tena,* hakuna hata mmoja wao aliyesikiliza ili kupokea nidhamu.+ 34 Nao waliweka sanamu zao zinazochukiza katika nyumba inayoitwa kwa jina langu, ili kuitia unajisi.+ 35 Isitoshe, walijenga mahali pa juu pa Baali katika Bonde la Mwana wa Hinomu,*+ ili kuwateketeza* motoni wana wao na mabinti wao kwa ajili ya Moleki,+ jambo ambalo sikuwaamuru,+ na ambalo halijawahi kamwe kuingia moyoni mwangu,* kufanya jambo kama hilo linalochukiza, na kusababisha watu wa Yuda watende dhambi.’

36 “Kwa hiyo Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi kuhusu jiji hili ambalo mnasema litatiwa mikononi mwa mfalme wa Babiloni kwa upanga, kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari, 37 ‘Nitawakusanya pamoja kutoka katika nchi zote ambako niliwatawanya kwa hasira yangu na kwa ghadhabu yangu na kwa ukali mwingi,+ nami nitawarudisha mahali hapa na kufanya wakae kwa usalama.+ 38 Nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao.+ 39 Nami nitawapa moyo mmoja+ na njia moja ili waniogope sikuzote, kwa faida yao wenyewe na kwa faida ya watoto wao baada yao.+ 40 Nami nitafanya pamoja nao agano linalodumu milele,+ kwamba sitaacha kuwatendea mema;+ nami nitatia hofu yangu katika mioyo yao, hivi kwamba hawataniacha.+ 41 Nitafurahia kuwatendea mema,+ nami nitawapanda kwa uthabiti katika nchi hii,+ kwa moyo wangu wote na kwa nafsi* yangu yote.’”

42 “Kwa maana Yehova anasema hivi: ‘Kama nilivyowaletea watu hawa msiba huu mkubwa, ndivyo nitakavyowaletea mema yote ninayowaahidi.*+ 43 Na mashamba yatanunuliwa tena katika nchi hii,+ ingawa mnasema: “Ni nchi yenye ukiwa isiyo na mwanadamu wala mnyama, nayo imetiwa mikononi mwa Wakaldayo.”’

44 “‘Mashamba yatanunuliwa kwa pesa, hati za ununuzi zitaandikwa na kutiwa muhuri, nao mashahidi wataitwa katika nchi ya Benjamini,+ katika maeneo yanayozunguka Yerusalemu, katika majiji ya Yuda,+ katika majiji ya eneo lenye milima, na katika majiji ya eneo la chini,+ na katika majiji ya kusini, kwa sababu nitawarudisha mateka wao,’+ asema Yehova.”

33 Neno la Yehova likamjia Yeremia mara ya pili, alipokuwa bado amezuiliwa katika Ua wa Walinzi,+ na kusema: 2 “Yehova, Muumba wa dunia, anasema hivi, Yehova aliyeiumba na kuifanya imara kabisa; Yehova ndilo jina lake, 3 ‘Niite, nami nitakujibu na kukuambia kwa utayari mambo makubwa na yasiyoeleweka ambayo hujayajua.’”+

4 “Kwa maana Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi kuhusu nyumba za jiji hili na kuhusu nyumba za wafalme wa Yuda ambazo zimebomolewa kwa sababu ya maboma ya kuzingira na kwa sababu ya upanga,+ 5 na kuhusu wale wanaokuja kupigana na Wakaldayo, na kujaza maeneo haya mizoga ya wale niliowaua katika hasira yangu na katika ghadhabu yangu, wale ambao uovu wao umenifanya niufiche uso wangu kutoka kwenye jiji hili: 6 ‘Ninamponya na kumpa afya,+ nami nitawaponya na kuwafunulia wingi wa amani na kweli.+ 7 Nami nitawarudisha mateka wa Yuda na mateka wa Israeli,+ nami nitawajenga kama nilivyofanya mwanzoni.+ 8 Nami nitawatakasa kutokana na hatia yote ya dhambi walizonitendea,+ nami nitasamehe hatia yote ya dhambi zao na makosa waliyonikosea.+ 9 Naye atakuwa kwangu jina la furaha, sifa, na uzuri mbele ya mataifa yote ya dunia yatakayosikia kuhusu wema wote nitakaowapa.+ Nao wataogopa na kutetemeka+ kwa sababu ya wema na amani ninayompa.’”+

10 “Yehova anasema hivi, ‘Mahali hapa ambapo mtasema ni nchi iliyo ukiwa, isiyo na wanadamu wala mifugo, katika majiji ya Yuda na katika barabara za Yerusalemu zilizo tupu, bila wanadamu wala wakaaji wala mifugo, itasikika tena 11 sauti ya furaha na sauti ya shangwe,+ sauti ya bwana harusi na sauti ya bibi harusi, sauti ya wale wanaosema: “Mshukuruni Yehova wa majeshi, kwa maana Yehova ni mwema;+ upendo wake mshikamanifu unadumu milele!”’+

“‘Wataleta matoleo ya shukrani katika nyumba ya Yehova,+ kwa maana nitawarudisha mateka wa nchi, kama hapo mwanzoni,’ asema Yehova.”

12 “Yehova wa majeshi anasema hivi, ‘Katika eneo hili lenye ukiwa, lisilo na mtu au mifugo, na katika majiji yake yote kutakuwa tena na malisho kwa ajili ya wachungaji kupumzisha makundi yao.’+

13 “‘Katika majiji ya eneo lenye milima, katika majiji ya eneo la chini, katika majiji ya kusini, katika nchi ya Benjamini, katika maeneo yanayozunguka Yerusalemu+ na katika majiji ya Yuda,+ makundi yatapita tena chini ya mikono ya mtu anayeyahesabu,’ asema Yehova.”

14 “‘Tazama! Siku zinakuja,’ asema Yehova, ‘nitakapotimiza ahadi nzuri niliyotoa kuhusu nyumba ya Israeli na nyumba ya Yuda.+ 15 Siku hizo na wakati huo nitamchipushia Daudi chipukizi adilifu,*+ naye atatenda haki na uadilifu katika nchi.+ 16 Siku hizo Yuda ataokolewa+ na Yerusalemu litakaa katika usalama.+ Naye ataitwa: Yehova Ni Uadilifu Wetu.’”+

17 “Kwa maana Yehova anasema hivi, ‘Hutakosa kamwe mwanamume wa ukoo wa Daudi atakayeketi kwenye kiti cha ufalme cha nyumba ya Israeli,+ 18 wala makuhani Walawi hawatakosa mtu wa kusimama mbele zangu ili kutoa dhabihu nzima za kuteketeza, kuchoma matoleo ya nafaka, na kutoa dhabihu.’”

19 Nalo neno la Yehova likamjia Yeremia tena, na kusema: 20 “Yehova anasema hivi, ‘Ikiwa mngeweza kulivunja agano langu kuhusu mchana na agano langu kuhusu usiku, ili kuzuia mchana na usiku usije kwa wakati wake,+ 21 hapo ndipo agano langu pamoja na mtumishi wangu Daudi lingeweza kuvunjwa,+ ili asiwe na mwana anayetawala akiwa mfalme kwenye kiti chake cha ufalme,+ na pia agano langu pamoja na makuhani, Walawi, wahudumu wangu.+ 22 Kama jeshi la mbinguni lisivyoweza kuhesabiwa wala mchanga wa bahari usivyoweza kupimwa, ndivyo nitakavyouzidisha uzao wa* mtumishi wangu Daudi na Walawi wanaonihudumia.’”

23 Nalo neno la Yehova likamjia tena Yeremia, na kusema: 24 “Je, hujasikia yale ambayo watu hawa wanasema, ‘Yehova atazikataa familia mbili alizozichagua’? Nao wanawavunjia heshima watu wangu, na hawawatambui tena kuwa taifa.

25 “Yehova anasema hivi: ‘Kwa hakika kama nilivyoweka imara agano langu kuhusu mchana na usiku,+ sheria za* mbingu na dunia,+ 26 vivyo hivyo sitaukataa kamwe uzao wa* Yakobo na wa mtumishi wangu Daudi, hivi kwamba nisichukue kutoka kwa uzao wake* watawala wa wazao wa* Abrahamu, Isaka, na Yakobo. Kwa maana nitawakusanya mateka wao+ na kuwahurumia.’”+

34 Neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Yehova, Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni na jeshi lake lote na falme zote za dunia chini ya mamlaka yake na mataifa yote yalipokuwa yakishambulia Yerusalemu na majiji yake yote:+

2 “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Nenda uzungumze na Mfalme Sedekia+ wa Yuda nawe umwambie hivi: “Yehova anasema, ‘Ninalitia jiji hili mikononi mwa mfalme wa Babiloni, naye ataliteketeza kwa moto.+ 3 Nawe hutaponyoka kutoka mikononi mwake, kwa maana kwa hakika utakamatwa na kutiwa mikononi mwake.+ Nawe utamwona Mfalme wa Babiloni jicho kwa jicho, naye atazungumza nawe uso kwa uso, nawe utapelekwa Babiloni.’+ 4 Hata hivyo, sikia neno la Yehova, ewe Mfalme Sedekia wa Yuda, ‘Yehova anasema hivi kukuhusu wewe: “Hutakufa kwa upanga. 5 Utakufa kwa amani,+ nao watakufanyia sherehe ya kufukiza manukato kama walivyowafanyia baba zako, wafalme wa zamani waliokutangulia, nao watakuombolezea wakisema, ‘Ole, ewe bwana!’ kwa maana ‘nimelisema neno hilo,’ asema Yehova.”’”’”

6 Kisha nabii Yeremia akamwambia maneno haya yote Mfalme Sedekia wa Yuda huko Yerusalemu, 7 majeshi ya mfalme wa Babiloni yalipokuwa yakishambulia Yerusalemu na majiji yote ya Yuda yaliyobaki,+ yakishambulia Lakishi+ na Azeka;+ kwa maana hayo ndiyo majiji pekee ya Yuda yenye ngome yaliyobaki.

8 Neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Yehova baada ya Mfalme Sedekia kufanya agano pamoja na watu wote waliokuwa Yerusalemu ili kuwatangazia uhuru,+ 9 kwamba kila mtu awaachilie huru watumwa wake Waebrania, wa kiume na wa kike, ili mtu yeyote asimfanye Myahudi mwenzake kuwa mtumwa. 10 Basi wakuu wote na watu wote wakatii. Walikuwa wamefanya agano kwamba kila mtu awaachilie huru watumwa wake wa kiume na wa kike na asiwafanye tena kuwa watumwa. Wakatii na kuwaruhusu waende zao. 11 Hata hivyo, baadaye waliwarudisha watumwa wao wa kiume na wa kike ambao walikuwa wamewaachilia huru, nao wakawalazimisha tena kuwa watumwa. 12 Basi neno la Yehova likamjia Yeremia kutoka kwa Yehova likisema:

13 “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Nilifanya agano pamoja na mababu zenu+ siku niliyowatoa nchini Misri, kutoka katika nyumba ya utumwa,+ nikisema: 14 “Mwishoni mwa miaka saba, kila mmoja wenu anapaswa kumwachilia huru ndugu yake Mwebrania aliyeuzwa kwake na ambaye amemtumikia miaka sita; lazima umwachilie huru.”+ Lakini mababu zenu hawakunisikiliza wala kunitegea masikio yao. 15 Na hivi karibuni* ninyi wenyewe mligeuka na kufanya yaliyo sawa machoni pangu kwa kuwatangazia uhuru wenzenu, nanyi mkafanya agano mbele zangu katika nyumba inayoitwa kwa jina langu. 16 Lakini mligeuka tena na kulichafua jina langu+ kwa kuwarudisha watumwa wenu wa kiume na wa kike ambao mlikuwa mmewaachilia huru kama walivyotaka, nanyi mkawalazimisha tena kuwa watumwa.’

17 “Kwa hiyo Yehova anasema hivi: ‘Hamjanitii kwa sababu kila mtu hajamtangazia uhuru ndugu yake na mwenzake.+ Basi sasa ninawatangazia uhuru,’ asema Yehova, ‘kwa upanga, ugonjwa hatari, na njaa kali,+ nami nitawafanya muwe kitu cha kutisha kwa falme zote za dunia.+ 18 Na hivi ndivyo itakavyokuwa kwa watu waliolivunja agano langu kwa kutofuata maneno ya agano walilofanya mbele zangu walipomkata ndama vipande viwili na kupita kati ya vile vipande viwili,+ 19 yaani, wakuu wa Yuda, wakuu wa Yerusalemu, maofisa wa makao ya mfalme, makuhani, na watu wote wa nchi waliopita kati ya vile vipande viwili vya ndama: 20 Nitawatia mikononi mwa maadui wao na mikononi mwa wale wanaotaka kuwaua,* na maiti zao zitakuwa chakula cha ndege wa angani na cha wanyama wa dunia.+ 21 Nami nitamtia Mfalme Sedekia wa Yuda na wakuu wake mikononi mwa maadui wao na mikononi mwa wale wanaotaka kuwaua* na mikononi mwa majeshi ya mfalme wa Babiloni,+ ambao wanaondoka na kuacha kuwashambulia.’+

22 “‘Nitatoa agizo,’ asema Yehova, ‘nami nitawarudisha katika jiji hili, nao watalishambulia na kuliteka na kuliteketeza kwa moto;+ nami nitayafanya majiji ya Yuda yawe ukiwa, bila mkaaji.’”+

35 Neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Yehova katika siku za Yehoyakimu+ mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda likisema: 2 “Nenda katika nyumba ya Warekabu+ na uzungumze nao na kuwaleta katika nyumba ya Yehova, katika mojawapo ya vyumba vya kulia chakula;* nawe uwape divai wanywe.”

3 Basi nikampeleka Yaazania mwana wa Yeremia mwana wa Habasinia, ndugu zake, wanawe wote, na nyumba yote ya Warekabu 4 kwenye nyumba ya Yehova. Niliwapeleka katika chumba cha kulia chakula cha wana wa Hanani mwana wa Igdalia, mtu wa Mungu wa kweli, kilichokuwa kando ya chumba cha kulia chakula cha wakuu ambacho kilikuwa juu ya chumba cha kulia chakula cha Maaseya mwana wa Shalumu mlinzi wa mlango. 5 Kisha nikaweka vikombe na bilauri zilizojaa divai mbele ya watu wa nyumba ya Warekabu na kuwaambia: “Kunyweni divai.”

6 Lakini wakasema: “Hatutakunywa divai, kwa sababu Yehonadabu*+ mwana wa Rekabu, babu yetu, alituamuru hivi: ‘Ninyi wala wana wenu hampaswi kamwe kunywa divai. 7 Nanyi hampaswi kujenga nyumba, kupanda mbegu, au kupanda shamba la mizabibu au kulimiliki. Badala yake, mnapaswa kukaa katika mahema sikuzote, ili mwishi kwa muda mrefu katika nchi mnayoishi ndani yake mkiwa wageni.’ 8 Basi tunaendelea kuitii sauti ya Yehonadabu mwana wa Rekabu babu yetu kuhusu mambo yote aliyotuamuru, kwa kutokunywa kamwe divai—sisi, wake zetu, wana wetu, na mabinti wetu. 9 Nasi hatujengi nyumba za kuishi humo, wala hatuna mizabibu wala mashamba wala mbegu. 10 Tunaendelea kuishi katika mahema na kutii mambo yote ambayo babu yetu Yehonadabu* alituamuru. 11 Lakini Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni alipoishambulia nchi,+ tukasema, ‘Njooni, tuingie ndani ya Yerusalemu ili kuepuka jeshi la Wakaldayo na la Wasiria, na sasa tunaishi Yerusalemu.’”

12 Na neno la Yehova likamjia Yeremia likisema: 13 “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Nenda uwaambie watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu: “Je, hamkuendelea kuhimizwa myatii maneno yangu?”+ asema Yehova. 14 “Yehonadabu mwana wa Rekabu aliwaamuru wazao wake wasinywe divai, nao wamefuata maneno yake kwa kutokunywa divai mpaka leo hii, na hivyo wameitii amri ya babu yao.+ Hata hivyo, nimezungumza nanyi tena na tena,* lakini hamjatii.+ 15 Nami niliendelea kuwatuma kwenu watumishi wangu wote manabii, nikiwatuma tena na tena,*+ na kusema, ‘Tafadhali geukeni, kila mmoja wenu kutoka kwenye njia zenu za uovu,+ nanyi mfanye yaliyo sawa! Msifuate miungu mingine na kuiabudu. Ndipo mtakapoendelea kukaa katika nchi niliyowapa ninyi na mababu zenu.’+ Lakini hamkutega sikio lenu wala hamkunisikiliza. 16 Wazao wa Yehonadabu mwana wa Rekabu wamefuata agizo ambalo babu yao aliwapa,+ lakini watu hawa hawajanisikiliza.”’”

17 “Kwa hiyo Yehova, Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Ninawaletea watu wa Yuda na wakaaji wote wa Yerusalemu msiba wote niliowaonya kuuhusu,+ kwa maana nimezungumza nao, lakini walikataa kusikiliza, nami nikaendelea kuwaita, lakini walikataa kujibu.’”+

18 Naye Yeremia akawaambia hivi watu wa nyumba ya Warekabu: “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Kwa sababu mmetii agizo la babu yenu Yehonadabu nanyi mnaendelea kufuata maagizo yake yote, na kufanya sawasawa na alivyowaagiza, 19 Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Hatakosekana kamwe mzao wa Yehonadabu* mwana wa Rekabu atakayetumikia mbele zangu.”’”

36 Sasa katika mwaka wa nne wa utawala wa Yehoyakimu+ mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, neno hili lilimjia Yeremia kutoka kwa Yehova likisema: 2 “Chukua kitabu cha kukunjwa na uandike ndani yake maneno yote ambayo nimekuambia dhidi ya Israeli na Yuda+ na mataifa yote,+ tangu siku ya kwanza niliyozungumza nawe katika siku za utawala wa Yosia mpaka leo hii.+ 3 Labda watu wa nyumba ya Yuda watakaposikia kuhusu msiba wote ninaokusudia kuwaletea, wataziacha njia zao za uovu, ili niwasamehe kosa lao na dhambi yao.”+

4 Kisha Yeremia akamwita Baruku+ mwana wa Neria, naye Yeremia akamwambia maneno yote ambayo Yehova alikuwa amemwambia, naye Baruku akayaandika maneno hayo katika kitabu cha kukunjwa Yeremia alipokuwa akiyasema.+ 5 Kisha Yeremia akamwamuru Baruku: “Nimezuiliwa, siwezi kuingia katika nyumba ya Yehova. 6 Basi wewe ndiye utakayeingia na kusoma kwa sauti maneno ya Yehova yaliyo katika kitabu cha kukunjwa ulichoandika nilipokuwa nikiyasema. Yasome watu wakisikia katika nyumba ya Yehova siku ya kufunga; basi utawasomea watu wote wa Yuda wanaokuja kutoka katika majiji yao. 7 Labda ombi lao la kutaka kibali litamfikia Yehova, nao watageuka, kila mtu kutoka katika njia zake za uovu, kwa maana Yehova amewatangazia watu hawa hasira na ghadhabu kubwa.”

8 Basi Baruku mwana wa Neria akafanya yote ambayo nabii Yeremia alimwamuru; akasoma kwa sauti maneno ya Yehova yaliyokuwa katika kile kitabu cha kukunjwa kwenye nyumba ya Yehova.+

9 Katika mwaka wa tano wa utawala wa Yehoyakimu+ mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, katika mwezi wa tisa, watu wote wa Yerusalemu na watu wote waliokuja Yerusalemu kutoka katika majiji ya Yuda wakatangaza watu wafunge mbele za Yehova.+ 10 Kisha Baruku akasoma kwa sauti maneno ya Yeremia yaliyokuwa katika kile kitabu cha kukunjwa kwenye nyumba ya Yehova, katika chumba* cha Gemaria+ mwana wa Shafani+ mwandishi,* katika ua wa juu, kwenye njia inayoelekea kwenye lango jipya la nyumba ya Yehova,+ watu wote wakisikia.

11 Mikaya mwana wa Gemaria mwana wa Shafani alipoyasikia maneno yote ya Yehova kutoka katika kile kitabu cha kukunjwa, 12 akashuka kwenda kwenye nyumba ya* mfalme, katika chumba cha mwandishi. Wakuu wote* walikuwa wameketi humo: mwandishi Elishama,+ Delaya mwana wa Shemaya, Elnathani+ mwana wa Akbori,+ Gemaria mwana wa Shafani, Sedekia mwana wa Hanania, na wakuu wengine wote. 13 Mikaya akawaambia maneno yote aliyokuwa ameyasikia Baruku aliposoma kile kitabu cha kukunjwa mbele ya watu.

14 Ndipo wakuu wote wakamtuma Yehudi mwana wa Nethania mwana wa Shelemia mwana wa Kushi kwa Baruku, wakisema: “Njoo na kitabu cha kukunjwa ulichosoma mbele ya watu.” Baruku mwana wa Neria akabeba kile kitabu cha kukunjwa mkononi mwake na kuingia walimokuwa. 15 Wakamwambia: “Tafadhali keti, nawe utusomee kitabu hicho kwa sauti.” Basi Baruku akawasomea kitabu hicho.

16 Sasa mara tu walipoyasikia maneno hayo yote, wakaangaliana kwa hofu, nao wakamwambia Baruku: “Lazima tumwambie mfalme maneno haya yote.” 17 Nao wakamuuliza Baruku: “Tafadhali tuambie jinsi ulivyoandika maneno haya yote. Je, aliyasema huku ukiandika?” 18 Baruku akawajibu: “Aliniambia maneno haya yote, nami nikayaandika kwa wino katika kitabu hiki cha kukunjwa.” 19 Wakuu wakamwambia Baruku: “Nenda ujifiche, wewe pamoja na Yeremia, na msiache mtu yeyote ajue mahali mlipo.”+

20 Kisha wakaingia kwa mfalme, kwenye ua, na kukiweka kitabu hicho cha kukunjwa kwenye chumba cha mwandishi Elishama, nao wakamwambia mfalme kila kitu walichosikia.

21 Basi mfalme akamtuma Yehudi+ aende kuleta kitabu hicho cha kukunjwa, naye akakileta kutoka katika chumba cha mwandishi Elishama. Yehudi akaanza kukisoma mbele ya mfalme na wakuu wote waliokuwa wamesimama karibu na mfalme. 22 Mfalme alikuwa ameketi katika nyumba ya majira ya baridi kali, katika mwezi wa tisa,* huku jiko la makaa likiwaka mbele yake. 23 Kila mara Yehudi aliposoma safu tatu au nne, mfalme aliikata sehemu hiyo kwa kisu cha mwandishi na kuitupa ndani ya moto katika jiko la makaa, mpaka kitabu chote cha kukunjwa kilipoteketea katika jiko hilo. 24 Nao hawakushikwa na hofu yoyote; wala mfalme wala watumishi wake wote waliosikia maneno hayo hawakuyararua mavazi yao. 25 Ingawa Elnathani,+ Delaya,+ na Gemaria+ walimsihi mfalme asikiteketeze kitabu hicho cha kukunjwa, hakuwasikiliza. 26 Isitoshe, mfalme akawaamuru Yerahmeeli mwana wa mfalme, Seraya mwana wa Azrieli, na Shelemia mwana wa Abdeeli wamkamate mwandishi Baruku na nabii Yeremia, lakini Yehova akaendelea kuwaficha.+

27 Na neno hili la Yehova likamjia Yeremia tena baada ya mfalme kukiteketeza kile kitabu cha kukunjwa kilichokuwa na maneno ambayo Baruku aliyaandika Yeremia alipokuwa akiyasema:+ 28 “Chukua kitabu kingine cha kukunjwa nawe uandike ndani yake maneno yaleyale yaliyokuwa kwenye kile kitabu cha kwanza cha kukunjwa, ambacho Mfalme Yehoyakimu wa Yuda alikiteketeza.+ 29 Nawe unapaswa kusema hivi dhidi ya Mfalme Yehoyakimu wa Yuda: ‘Yehova anasema hivi: “Umekiteketeza kitabu hiki cha kukunjwa na kusema, ‘Kwa nini umeandika ndani yake, “Mfalme wa Babiloni atakuja hakika na kuiharibu nchi hii na kumwangamiza mwanadamu na mnyama kutoka humu”?’+ 30 Kwa hiyo Yehova anasema hivi dhidi ya Mfalme Yehoyakimu wa Yuda, ‘Hatakuwa na mtu yeyote atakayeketi kwenye kiti cha ufalme cha Daudi,+ na maiti yake itaachwa nje kwenye joto wakati wa mchana na baridi kali wakati wa usiku.+ 31 Nitamwadhibu yeye na wazao wake* na watumishi wake kwa sababu ya kosa lao, nami nitawaletea wao na wakaaji wa Yerusalemu na watu wa Yuda msiba wote niliotangaza dhidi yao,+ lakini hawakusikiliza.’”’”+

32 Kisha Yeremia akachukua kitabu kingine cha kukunjwa na kumpa Baruku mwana wa Neria, mwandishi,+ naye akaandika maneno yote aliyoambiwa na Yeremia ambayo yalikuwa katika kile kitabu cha kukunjwa ambacho Mfalme Yehoyakimu wa Yuda alikuwa amekiteketeza motoni.+ Na maneno mengine mengi kama hayo yakaongezwa.

37 Na Mfalme Sedekia+ mwana wa Yosia akaanza kutawala baada ya Konia*+ mwana wa Yehoyakimu, kwa maana Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni alikuwa amemweka kuwa mfalme katika nchi ya Yuda.+ 2 Lakini yeye na watumishi wake na watu wa nchi hawakuyasikiliza maneno ya Yehova yaliyosemwa kupitia nabii Yeremia.

3 Na Mfalme Sedekia akamtuma Yehukali+ mwana wa Shelemia na Sefania+ mwana wa kuhani Maaseya kwa nabii Yeremia, akisema: “Tafadhali sali kwa ajili yetu kwa Yehova Mungu wetu.” 4 Yeremia alikuwa akitembea kwa uhuru miongoni mwa watu, kwa maana bado hakuwa ametiwa gerezani.+ 5 Sasa jeshi la Farao lilikuwa limeondoka Misri,+ na Wakaldayo waliokuwa wakizingira Yerusalemu wakasikia habari kulihusu. Basi wakaondoka Yerusalemu.+ 6 Kisha neno la Yehova likamjia nabii Yeremia likisema: 7 “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Mnapaswa kumwambia hivi mfalme wa Yuda, aliyewatuma kwangu kutafuta habari: “Tazama! Jeshi la Farao linalokuja kuwasaidia litalazimika kurudi nchini kwao, Misri.+ 8 Na Wakaldayo watarudi tena na kulishambulia jiji hili na kuliteka na kuliteketeza kwa moto.”+ 9 Yehova anasema hivi: “Msijidanganye* kwa kusema, ‘Hakika Wakaldayo wataondoka na kutuacha,’ kwa sababu hawataondoka. 10 Hata kama mngeliangamiza jeshi lote la Wakaldayo wanaopigana nanyi na wabaki tu wale waliojeruhiwa, bado wangetoka katika mahema yao na kuliteketeza jiji hili kwa moto.”’”+

11 Jeshi la Wakaldayo lilipoondoka Yerusalemu kwa sababu ya jeshi la Farao,+ 12 Yeremia akaondoka Yerusalemu na kwenda kwenye nchi ya Benjamini+ ili apate fungu lake huko miongoni mwa watu wake. 13 Lakini alipofika kwenye Lango la Benjamini, ofisa aliyesimamia walinzi, aliyeitwa Iriya mwana wa Shelemia mwana wa Hanania, akamkamata nabii Yeremia na kumwambia: “Unakimbia kwenda kwa Wakaldayo!” 14 Lakini Yeremia akasema: “Si kweli! Mimi sikimbii kwenda kwa Wakaldayo.” Lakini hakumsikiliza. Basi Iriya akamkamata Yeremia na kumpeleka kwa wakuu. 15 Wakuu wakamkasirikia vikali Yeremia,+ nao wakampiga na kumfunga*+ katika nyumba ya mwandishi Yehonathani, iliyokuwa imefanywa kuwa gereza. 16 Yeremia alitiwa katika gereza lililo chini ya ardhi,* kwenye vyumba vyenye ngome, naye akakaa humo kwa siku nyingi.

17 Kisha Mfalme Sedekia akaagiza aletwe, naye mfalme akaanza kumuuliza maswali kisiri katika nyumba yake.*+ Akamuuliza, “Je, kuna neno lolote kutoka kwa Yehova?” Yeremia akasema: “Lipo!” naye akaendelea kusema: “Utatiwa mikononi mwa mfalme wa Babiloni!”+

18 Pia Yeremia akamwambia hivi Mfalme Sedekia: “Nimekutendea dhambi gani wewe na watumishi wako na watu hawa, hivi kwamba mmenifunga gerezani? 19 Wako wapi sasa manabii wenu waliowatabiria kwamba ‘Mfalme wa Babiloni hatakushambulia wewe wala nchi hii’?+ 20 Sasa sikiliza, tafadhali, ewe bwana wangu mfalme. Tafadhali, kubali ombi langu la kupata kibali. Usinirudishe katika nyumba ya mwandishi Yehonathani,+ la sivyo nitafia humo.”+ 21 Basi Mfalme Sedekia akaamuru Yeremia awekwe kifungoni katika Ua wa Walinzi,+ naye alipewa mkate wa mviringo kila siku kutoka kwenye barabara ya waokaji+ mpaka mikate yote ilipokwisha jijini.+ Na Yeremia akaendelea kukaa katika Ua wa Walinzi.

38 Sasa Shefatia mwana wa Matani, Gedalia mwana wa Pashuri, Yukali+ mwana wa Shelemia, na Pashuri+ mwana wa Malkiya wakasikia maneno ambayo Yeremia alikuwa akiwaambia watu wote, akisema: 2 “Yehova anasema hivi: ‘Yule atakayebaki katika jiji hili atakufa kwa upanga, kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari.+ Lakini yule atakayejisalimisha* kwa Wakaldayo ataendelea kuishi naye atapata uhai wake* kama nyara* na kuendelea kuishi.’+ 3 Yehova anasema hivi: ‘Kwa kweli jiji hili litatiwa mikononi mwa jeshi la mfalme wa Babiloni, naye ataliteka.’”+

4 Wakuu wakamwambia mfalme: “Tafadhali agiza mtu huyu auawe,+ kwa maana hivyo ndivyo anavyoidhoofisha mioyo* ya wanajeshi waliobaki jijini, na pia ya watu wote, kwa kuwaambia maneno hayo. Kwa maana mtu huyu hawatakii amani watu hawa, bali msiba.” 5 Mfalme Sedekia akajibu: “Tazama! Yuko mikononi mwenu, kwa maana mfalme hawezi kufanya jambo lolote ili kuwazuia.”

6 Basi wakamchukua Yeremia na kumtupa ndani ya tangi la maji la Malkiya mwana wa mfalme, lililokuwa katika Ua wa Walinzi.+ Wakamshusha Yeremia ndani kwa kamba. Basi hapakuwa na maji ndani ya tangi hilo, ila matope tu, naye Yeremia akaanza kuzama ndani ya matope.

7 Ebed-meleki+ Mwethiopia, towashi* aliyekuwa katika nyumba ya* mfalme, akasikia kwamba wamemtia Yeremia ndani ya tangi. Sasa mfalme alikuwa ameketi katika Lango la Benjamini,+ 8 basi Ebed-meleki akatoka katika nyumba ya* mfalme na kuzungumza na mfalme, akisema: 9 “Ee bwana wangu mfalme, watu hawa wamemtendea Yeremia uovu! Wamemtupa ndani ya tangi, naye atafia humo kwa sababu ya njaa kali, kwa maana hakuna mkate uliobaki jijini.”+

10 Ndipo mfalme akamwamuru hivi Ebed-meleki Mwethiopia: “Chukua watu 30 kutoka mahali hapa, nawe umvute nabii Yeremia kutoka katika tangi hilo kabla hajafa.” 11 Basi Ebed-meleki akawachukua wale watu na kwenda kwenye nyumba ya* mfalme sehemu iliyokuwa chini ya hazina,+ naye akachukua kutoka sehemu hiyo matambara yaliyochakaa na vipande vya nguo vilivyochakaa na kumshushia Yeremia ndani ya tangi hilo kwa kamba. 12 Ndipo Ebed-meleki Mwethiopia akamwambia Yeremia: “Tafadhali weka matambara na vipande hivyo vya nguo kati ya makwapa yako na kamba.” Yeremia akafanya hivyo, 13 nao wakamvuta Yeremia nje kwa zile kamba na kumtoa ndani ya tangi hilo. Na Yeremia akaendelea kukaa katika Ua wa Walinzi.+

14 Mfalme Sedekia akaagiza Yeremia aletwe kwake kwenye mlango wa tatu, ulio katika nyumba ya Yehova, naye mfalme akamwambia Yeremia: “Ningependa kukuuliza jambo fulani. Usinifiche jambo lolote.” 15 Ndipo Yeremia akamwambia Sedekia: “Nikikuambia, kwa kweli utaniua. Nami nikikushauri, hutanisikiliza.” 16 Basi Mfalme Sedekia akamwapia Yeremia kisiri, akisema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, ambaye ametupatia uhai huu, sitakuua, nami sitakutia mikononi mwa watu hawa wanaotaka kukuua.”*

17 Kisha Yeremia akamwambia Sedekia: “Yehova, Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Ukijisalimisha* kwa wakuu wa mfalme wa Babiloni, uhai wako utaokoka,* na jiji hili halitateketezwa kwa moto, na wewe na watu wa nyumba yako mtaokoka.+ 18 Lakini usipojisalimisha* kwa wakuu wa mfalme wa Babiloni, jiji hili litatiwa mikononi mwa Wakaldayo, nao wataliteketeza kwa moto,+ nawe hutaponyoka mikononi mwao.’”+

19 Kisha Mfalme Sedekia akamwambia Yeremia: “Ninawaogopa Wayahudi ambao wamekimbia kwenda kwa Wakaldayo, kwa maana nikitiwa mikononi mwao watanitendea ukatili.” 20 Lakini Yeremia akasema: “Hutatiwa mikononi mwao. Tafadhali, itii sauti ya Yehova kuhusiana na yale ninayokuambia, na mambo yatakuendea vema, nawe utaendelea kuishi. 21 Lakini ukikataa kujisalimisha,* Yehova amenifunulia jambo hili: 22 Tazama! Wanawake wote waliobaki katika nyumba ya* mfalme wa Yuda wanatolewa nje kwa wakuu wa mfalme wa Babiloni,+ nao wanasema,

‘Watu uliowatumaini* wamekudanganya na kukushinda.+

Wamefanya mguu wako uzame kwenye matope.

Sasa wamegeuka na kurudi nyuma.’

23 Nao wanawatoa nje wake zako wote na wanao wote na kuwapeleka kwa Wakaldayo, nawe hutaponyoka mikononi mwao, lakini utakamatwa na mfalme wa Babiloni,+ na kwa sababu yako, jiji hili litateketezwa kwa moto.”+

24 Kisha Sedekia akamwambia Yeremia: “Usimwambie mtu yeyote mambo haya, ili usife. 25 Na wakuu wakisikia kwamba nimezungumza nawe nao waje na kukuambia, ‘Tafadhali, tuambie ulichomwambia mfalme. Usitufiche jambo lolote, nasi hatutakuua.+ Mfalme alikuambia nini?’ 26 utawajibu hivi: ‘Nilikuwa nikimwomba mfalme asinirudishe katika nyumba ya Yehonathani ili nisifie humo.’”+

27 Baadaye wakuu wote wakamjia Yeremia na kumuuliza maswali. Akawaambia mambo yote ambayo mfalme alimwamuru aseme. Basi hawakumwambia jambo lolote zaidi, kwa maana hakuna mtu aliyesikia mazungumzo hayo. 28 Mpaka siku ambayo Yerusalemu lilitekwa, Yeremia alikaa katika Ua wa Walinzi;+ bado alikuwa humo Yerusalemu lilipotekwa.+

39 Katika mwaka wa tisa wa utawala wa Mfalme Sedekia wa Yuda, katika mwezi wa kumi, Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni alikuja Yerusalemu na jeshi lake lote, na kulizingira jiji hilo.+

2 Katika mwaka wa 11 wa utawala wa Sedekia, mwezi wa nne, siku ya tisa ya mwezi huo, walibomoa sehemu ya ukuta wa jiji.+ 3 Na wakuu wote wa mfalme wa Babiloni wakaingia na kuketi katika Lango la Kati,+ yaani, Nergal-shareza yule Samgari, Nebo-sarsekimu yule Rabsarisi,* Nergal-shareza yule Rabmagi,* na wakuu wengine wote wa mfalme wa Babiloni.

4 Mfalme Sedekia wa Yuda na wanajeshi wote walipowaona walikimbia,+ wakatoka jijini wakati wa usiku kupitia njia ya bustani ya mfalme, kupitia lango lililokuwa kati ya kuta mbili, nao wakafuata njia inayoelekea Araba.+ 5 Lakini jeshi la Wakaldayo likawafuatia, nao wakamfikia Sedekia katika jangwa tambarare la Yeriko.+ Wakamkamata na kumleta kwa Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni kule Ribla+ katika nchi ya Hamathi,+ ambako alimhukumu. 6 Mfalme wa Babiloni akaagiza wana wa Sedekia wachinjwe mbele ya macho yake kule Ribla, na mfalme wa Babiloni akaagiza wakuu wote wa Yuda wachinjwe.+ 7 Ndipo akayapofusha macho ya Sedekia, kisha akamfunga kwa pingu za shaba ili ampeleke Babiloni.+

8 Halafu Wakaldayo wakaiteketeza nyumba ya* mfalme na nyumba za watu,+ nao wakazibomoa kabisa kuta za Yerusalemu.+ 9 Nebuzaradani+ mkuu wa walinzi akawapeleka uhamishoni kule Babiloni watu waliobaki jijini, na wale waliojisalimisha kwake, na yeyote aliyebaki.

10 Lakini Nebuzaradani mkuu wa walinzi aliwaacha katika nchi ya Yuda baadhi ya watu maskini kabisa, wale ambao hawakuwa na chochote. Siku hiyo aliwapatia pia mashamba ya mizabibu na mashamba mengine ili wayalime.*+

11 Ndipo Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni akamwagiza hivi Nebuzaradani mkuu wa walinzi kumhusu Yeremia: 12 “Mchukue nawe umtunze; usimdhuru, na umpe chochote atakachokuomba.”+

13 Basi Nebuzaradani mkuu wa walinzi, Nebushazbani yule Rabsarisi,* Nergal-shareza yule Rabmagi,* na wakuu wote wa mfalme wa Babiloni wakawatuma watu 14 wamtoe Yeremia katika Ua wa Walinzi+ na kumkabidhi kwa Gedalia+ mwana wa Ahikamu+ mwana wa Shafani+ ili apelekwe nyumbani kwake. Basi akaishi pamoja na watu wengine.

15 Yeremia alipokuwa amefungiwa katika Ua wa Walinzi,+ neno la Yehova lilimjia likisema: 16 “Nenda umwambie Ebed-meleki+ Mwethiopia, ‘Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Ninayatimiza maneno yangu kuhusu jiji hili ili kuleta msiba wala si mema, na siku hiyo utayaona yakitimia.”’

17 “‘Lakini nitakuokoa siku hiyo,’ asema Yehova, ‘nawe hutatiwa mikononi mwa watu unaowaogopa.’

18 “‘Kwa maana hakika nitakuokoa, nawe hutakufa kwa upanga. Uhai wako utakuwa* kama nyara,*+ kwa sababu ulinitumaini,’+ asema Yehova.”

40 Neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Yehova baada ya Nebuzaradani+ mkuu wa walinzi kumwachilia huru kutoka Rama.+ Alikuwa amempeleka huko akiwa amefungwa pingu mikononi, naye alikuwa miongoni mwa watu wote waliohamishwa kutoka Yerusalemu na Yuda waliokuwa wakipelekwa uhamishoni Babiloni. 2 Kisha mkuu wa walinzi akamchukua Yeremia na kumwambia: “Yehova Mungu wako alitabiri msiba huu dhidi ya mahali hapa, 3 na Yehova ameuleta msiba huo kama alivyosema, kwa sababu ninyi watu mlimtendea dhambi Yehova na hamkuitii sauti yake. Ndiyo sababu jambo hili limewapata.+ 4 Sasa ninakufungua pingu zilizo mikononi mwako. Ikiwa unaona ni vema kwako kwenda pamoja nami Babiloni, njoo, nami nitakutunza. Lakini ikiwa hutaki kwenda pamoja nami Babiloni, usije. Angalia! Nchi nzima iko mbele yako. Nenda popote unapotaka.”+

5 Hata kabla Yeremia hajageuka kuondoka, Nebuzaradani akamwambia: “Rudi kwa Gedalia+ mwana wa Ahikamu+ mwana wa Shafani,+ ambaye mfalme wa Babiloni amemweka juu ya majiji ya Yuda, nawe ukae pamoja naye miongoni mwa watu; au uende popote unapotaka.”

Ndipo mkuu wa walinzi akampa posho ya chakula na zawadi, akamruhusu aende zake. 6 Basi Yeremia akaenda kwa Gedalia mwana wa Ahikamu kule Mispa+ na kukaa pamoja naye miongoni mwa watu waliobaki nchini.

7 Baadaye wakuu wote wa majeshi waliokuwa uwanjani pamoja na watu wao wakasikia kwamba mfalme wa Babiloni amemweka Gedalia mwana wa Ahikamu awe msimamizi wa nchi na kwamba alikuwa amemweka awe msimamizi wa wanaume, wanawake, na watoto, watu maskini nchini ambao hawakuwa wamepelekwa uhamishoni Babiloni.+ 8 Basi wakaenda kwa Gedalia huko Mispa.+ Wakuu hao ni Ishmaeli+ mwana wa Nethania, Yohanani+ na Yonathani wana wa Karea, Seraya mwana wa Tanhumethi, wana wa Efai Mnetofa, na Yezania+ mwana wa Mmaakathi, pamoja na wanajeshi wao. 9 Gedalia mwana wa Ahikamu mwana wa Shafani akawaapia wao pamoja na wanajeshi wao, akisema: “Msiogope kuwatumikia Wakaldayo. Kaeni katika nchi hii na kumtumikia mfalme wa Babiloni, na mambo yatawaendea vema.+ 10 Lakini mimi, nitakaa Mispa, ili niwawakilishe kwa* Wakaldayo watakaokuja kwetu. Lakini ninyi mnapaswa kukusanya divai, matunda ya wakati wa kiangazi, na mafuta na kuviweka vitu hivyo katika vyombo vyenu vya kuhifadhia na mkae katika majiji mliyoyachukua.”+

11 Na Wayahudi wote waliokuwa Moabu, Amoni, na Edomu, na wale waliokuwa katika nchi nyingine zote, wakasikia pia kwamba mfalme wa Babiloni alikuwa amewaacha watu fulani wabaki Yuda na kwamba alikuwa amemweka Gedalia mwana wa Ahikamu mwana wa Shafani awe msimamizi wao. 12 Basi Wayahudi wote wakaanza kurudi kutoka kila mahali ambako walikuwa wametawanywa, nao wakaja katika nchi ya Yuda, kwa Gedalia huko Mispa. Nao wakakusanya divai na matunda ya wakati wa kiangazi kwa wingi sana.

13 Yohanani mwana wa Karea na wakuu wote wa jeshi waliokuwa uwanjani wakaja kwa Gedalia huko Mispa. 14 Wakamwambia: “Je, hujui kwamba Baalisi mfalme wa Waamoni,+ amemtuma Ishmaeli mwana wa Nethania akuue?”*+ Lakini Gedalia mwana wa Ahikamu hakuwaamini.

15 Kisha Yohanani mwana wa Karea akamwambia kisiri Gedalia huko Mispa: “Ninataka kwenda kumuua Ishmaeli mwana wa Nethania, na hakuna mtu atakayejua. Kwa nini akuue,* na kwa nini watu wote wa Yuda waliokusanyika kwako watawanyike na watu wa Yuda waliobaki waangamie?” 16 Lakini Gedalia+ mwana wa Ahikamu akamwambia Yohanani mwana wa Karea: “Usifanye hivyo, kwa maana unasema uwongo kumhusu Ishmaeli.”

41 Katika mwezi wa saba, Ishmaeli+ mwana wa Nethania mwana wa Elishama, aliyekuwa wa uzao wa kifalme* na mmoja kati ya wakuu wa mfalme, akaja pamoja na wanaume wengine kumi kwa Gedalia mwana wa Ahikamu huko Mispa.+ Walipokuwa wakila chakula pamoja huko Mispa, 2 Ishmaeli mwana wa Nethania na wale watu kumi waliokuwa pamoja naye wakasimama na kumpiga kwa upanga Gedalia mwana wa Ahikamu mwana wa Shafani. Kwa hiyo akamuua mtu ambaye mfalme wa Babiloni alikuwa amemweka kuwa msimamizi nchini. 3 Ishmaeli aliwaua pia Wayahudi wote waliokuwa pamoja na Gedalia huko Mispa, na pia wanajeshi Wakaldayo waliokuwa huko.

4 Siku ya pili baada ya Gedalia kuuawa, kabla mtu yeyote hajajua jambo hilo, 5 wakaja watu 80 kutoka Shekemu,+ kutoka Shilo,+ na kutoka Samaria.+ Ndevu zao zilikuwa zimenyolewa, mavazi yao yalikuwa yameraruka, walikuwa wamejikatakata,+ nao walikuwa na matoleo ya nafaka na uvumba+ mikononi mwao ili wavilete vitu hivyo katika nyumba ya Yehova. 6 Basi Ishmaeli mwana wa Nethania akatoka Mispa ili kuwapokea, naye alikuwa akitembea huku akilia. Alipokutana nao, akawaambia: “Njooni kwa Gedalia mwana wa Ahikamu.” 7 Lakini walipoingia jijini, Ishmaeli mwana wa Nethania na watu wake wakawachinja na kuwatupa ndani ya tangi la maji.

8 Lakini kulikuwa na watu kumi kati yao waliomwambia Ishmaeli: “Usituue, kwa maana shambani tuna maghala yaliyofichwa ya ngano, shayiri, mafuta, na asali.” Basi hakuwaua pamoja na ndugu zao. 9 Sasa Ishmaeli akazitupa maiti zote za watu aliowaua ndani ya tangi kubwa la maji, tangi ambalo Mfalme Asa alitengeneza kwa sababu ya Mfalme Baasha wa Israeli.+ Hilo ndilo tangi ambalo Ishmaeli mwana wa Nethania alilijaza maiti za watu waliouawa.

10 Ishmaeli akawachukua mateka watu wote waliobaki huko Mispa,+ kutia ndani mabinti wa mfalme na watu wote waliobaki Mispa, ambao Nebuzaradani mkuu wa walinzi alikuwa amewaweka chini ya ulinzi wa Gedalia+ mwana wa Ahikamu. Ishmaeli mwana wa Nethania aliwachukua mateka na kuvuka kwenda kwa Waamoni.+

11 Yohanani+ mwana wa Karea na wakuu wote wa jeshi waliokuwa pamoja naye waliposikia uovu wote ambao Ishmaeli mwana wa Nethania alikuwa ametenda, 12 wakawachukua wanaume wote na kwenda kupigana na Ishmaeli mwana wa Nethania, nao wakamkuta kando ya maji mengi* kule Gibeoni.

13 Watu wote waliokuwa pamoja na Ishmaeli wakashangilia walipomwona Yohanani mwana wa Karea na wakuu wote wa jeshi waliokuwa pamoja naye. 14 Ndipo watu wote ambao Ishmaeli alikuwa amewachukua mateka kutoka Mispa+ wakageuka na kurudi pamoja na Yohanani mwana wa Karea. 15 Lakini Ishmaeli mwana wa Nethania pamoja na wanaume wanane kati ya watu wake wakamtoroka Yohanani, na kwenda kwa Waamoni.

16 Yohanani mwana wa Karea na wakuu wote wa jeshi waliokuwa pamoja naye wakawachukua watu waliobaki Mispa ambao walikuwa wamewaokoa kutoka kwa Ishmaeli mwana wa Nethania baada ya kumuua Gedalia+ mwana wa Ahikamu. Wakawaleta wanaume, wanajeshi, wanawake, watoto, na maofisa wa makao ya mfalme kutoka Gibeoni. 17 Basi wakaenda na kukaa mahali pa kulala pa Kimhamu kando ya Bethlehemu,+ wakikusudia kwenda Misri,+ 18 kwa sababu ya Wakaldayo. Kwa maana waliwaogopa, kwa sababu Ishmaeli mwana wa Nethania alikuwa amemuua Gedalia mwana wa Ahikamu, ambaye mfalme wa Babiloni alikuwa amemweka kuwa msimamizi wa nchi.+

42 Kisha wakuu wote wa jeshi, na Yohanani+ mwana wa Karea, Yezania mwana wa Hoshaya, na watu wote, kuanzia mdogo zaidi mpaka mkubwa zaidi, wakakaribia 2 na kumwambia nabii Yeremia: “Tafadhali, sikia ombi letu la kutaka kibali nawe usali kwa ajili yetu kwa Yehova Mungu wako, kwa ajili ya watu hawa wote waliobaki, kwa maana kati ya watu wengi, wachache ndio waliobaki,+ kama unavyoona. 3 Yehova Mungu wako na atuambie njia tunayopaswa kuifuata na jambo tunalopaswa kufanya.”

4 Nabii Yeremia akawajibu: “Nimewasikia, nami ninasali kwa Yehova Mungu wenu kulingana na ombi lenu; na kila neno ambalo Yehova atawajibu, nitawaambia. Sitawaficha neno lolote.”

5 Wakamjibu Yeremia: “Yehova na awe shahidi wa kweli na mwaminifu dhidi yetu ikiwa hatutafanya sawasawa kama anavyotuagiza Yehova Mungu wako kupitia wewe. 6 Iwe ni jambo jema au baya, tutaitii sauti ya Yehova Mungu wetu ambaye tunakutuma kwake, ili mambo yatuendee vema kwa sababu tunaitii sauti ya Yehova Mungu wetu.”

7 Baada ya siku kumi neno la Yehova likamjia Yeremia. 8 Basi akamwita Yohanani mwana wa Karea na wakuu wote wa jeshi waliokuwa pamoja naye na watu wote, kuanzia mdogo zaidi mpaka mkubwa zaidi.+ 9 Akawaambia: “Yehova Mungu wa Israeli, ambaye mlinituma kwake ili kupeleka ombi lenu la kutaka kibali mbele zake, anasema hivi: 10 ‘Ikiwa kwa kweli mtakaa katika nchi hii, basi nitawajenga nami sitawabomoa, nitawapanda nami sitawang’oa, kwa maana nitaghairi* kuhusu msiba ambao nimewaletea.+ 11 Msimwogope mfalme wa Babiloni, mnayemwogopa.’+

“‘Msimwogope,’ asema Yehova, ‘kwa maana niko pamoja nanyi, ili kuwaokoa na kuwakomboa kutoka mikononi mwake. 12 Nami nitawaonyesha rehema,+ naye atawaonyesha rehema na kuwarudisha kwenye nchi yenu wenyewe.

13 “‘Lakini mkisema, “Hapana, hatutakaa katika nchi hii!” nanyi mkose kuitii sauti ya Yehova Mungu wenu 14 kwa kusema: “Hapana, badala yake tutaenda katika nchi ya Misri,+ ambako hatutaona vita wala kusikia sauti ya pembe wala kuwa na njaa kwa kukosa mkate; huko ndiko tutakakoishi,” 15 basi sikieni neno la Yehova, enyi watu wa Yuda mliobaki. Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Ikiwa mmeazimia kabisa kwenda Misri nanyi mwende kukaa huko,* 16 ndipo upanga uleule ambao mnaogopa utawafikia huko katika nchi ya Misri, na njaa ileile ambayo mnaogopa itawafuata huko Misri, nanyi mtafia huko.+ 17 Na watu wote walioazimia kwenda Misri ili kukaa huko watakufa kwa upanga, kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari. Hakuna yeyote kati yao atakayeokoka au kuponyoka msiba nitakaowaletea.”’

18 “Kwa maana Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Kama hasira yangu na ghadhabu yangu ilivyomwagwa juu ya wakaaji wa Yerusalemu,+ ndivyo ghadhabu yangu itakavyomwagwa juu yenu ikiwa mtaenda Misri, nanyi mtakuwa laana, kitu cha kutisha, matusi, na shutuma,+ nanyi hamtapaona tena kamwe mahali hapa.’

19 “Yehova amewakataza, enyi watu wa Yuda mliobaki. Msiende Misri. Mnapaswa kujua kwa hakika kwamba nimewaonya leo, 20 kwamba kosa lenu litawagharimu uhai wenu.* Kwa maana mlinituma kwa Yehova Mungu wenu, mkisema, ‘Sali kwa ajili yetu kwa Yehova Mungu wetu, nawe utuambie kila jambo ambalo Yehova Mungu wetu anasema, nasi tutalifanya.’+ 21 Nami nimewaambia leo, lakini hamtaitii sauti ya Yehova Mungu wenu wala kufanya jambo lolote alilonituma niwaambie.+ 22 Kwa hiyo, jueni kwa hakika kwamba mtakufa kwa upanga, kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari mahali mnapotamani kwenda kuishi.”+

43 Yeremia alipomaliza kuwaambia watu wote maneno hayo yote kutoka kwa Yehova Mungu wao, kila neno ambalo Yehova Mungu wao alikuwa amemtuma awaambie, 2 Azaria mwana wa Hoshaya, Yohanani+ mwana wa Karea, na watu wote wenye kimbelembele wakamwambia Yeremia: “Unasema uwongo! Yehova Mungu wetu hakukutuma useme, ‘Msiende kukaa Misri.’ 3 Lakini Baruku+ mwana wa Neria anakuchochea dhidi yetu ili kututia mikononi mwa Wakaldayo, ili watuue au kutupeleka uhamishoni Babiloni.”+

4 Basi Yohanani mwana wa Karea na wakuu wote wa jeshi na watu wote hawakuitii sauti ya Yehova kwamba wabaki katika nchi ya Yuda. 5 Badala yake, Yohanani mwana wa Karea na wakuu wote wa jeshi wakawachukua watu wote wa Yuda waliobaki ambao walikuwa wamerudi kuishi katika nchi ya Yuda kutoka katika mataifa yote ambako walikuwa wametawanywa.+ 6 Wakawachukua wanaume, wanawake, watoto, mabinti wa mfalme, na kila mtu ambaye Nebuzaradani+ mkuu wa walinzi alikuwa amemwacha pamoja na Gedalia+ mwana wa Ahikamu+ mwana wa Shafani,+ na pia nabii Yeremia na Baruku mwana wa Neria. 7 Nao wakaingia nchini Misri, kwa maana hawakuitii sauti ya Yehova, wakaenda mpaka Tahpanhesi.+

8 Kisha neno la Yehova likamjia Yeremia huko Tahpanhesi likisema: 9 “Beba mkononi mwako mawe makubwa, nawe uyafiche katika saruji kwenye ngazi ya matofali iliyo kwenye mlango wa nyumba ya Farao huko Tahpanhesi, huku wanaume Wayahudi wakitazama. 10 Kisha uwaambie, ‘Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Tazameni, ninamwita Nebukadneza* mfalme wa Babiloni, mtumishi wangu,+ nami nitakiweka kiti chake cha ufalme juu ya mawe haya ambayo nimeyaficha, naye atalitandaza hema lake la kifalme juu yake.+ 11 Naye ataingia na kuipiga nchi ya Misri.+ Yeyote aliyekusudiwa kufa kwa ugonjwa hatari atakufa kwa ugonjwa hatari, na yeyote aliyekusudiwa kwenda utekwani ataenda utekwani, na yeyote aliyekusudiwa kufa kwa upanga atakufa kwa upanga.+ 12 Nami nitaziwasha moto nyumba za* miungu ya Misri,+ naye ataiteketeza na kuichukua mateka. Atajifunika kwa nchi ya Misri kama mchungaji anavyojifunika kwa vazi lake, naye ataondoka huko kwa amani.* 13 Naye atazivunja vipandevipande nguzo za* Beth-shemeshi* katika nchi ya Misri, naye ataziteketeza kwa moto nyumba za* miungu ya Misri.”’”

44 Neno lililomjia Yeremia kwa ajili ya Wayahudi wote waliokuwa wakiishi katika nchi ya Misri,+ wale waliokuwa wakiishi Migdoli,+ Tahpanhesi,+ Nofu,*+ na katika nchi ya Pathrosi,+ likisema: 2 “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Mmeona msiba wote nilioleta dhidi ya Yerusalemu+ na dhidi ya majiji yote ya Yuda, na leo yamebaki magofu, bila mkaaji.+ 3 Ni kwa sababu ya mambo maovu waliyofanya ili kunikasirisha kwa kwenda kutoa dhabihu+ na kuiabudu miungu mingine ambayo hawakuijua, wala ninyi wala mababu zenu.+ 4 Niliendelea kuwatuma kwenu watumishi wangu wote manabii, niliwatuma tena na tena* nikisema: “Tafadhali msifanye jambo hili lenye kuchukiza ninalochukia.”+ 5 Lakini hawakusikiliza wala kutega sikio lao na kuacha uovu wao na kuacha kuitolea dhabihu miungu mingine.+ 6 Basi ghadhabu yangu na hasira yangu ilimwagwa na kuwaka katika majiji ya Yuda na kwenye barabara za Yerusalemu, na majiji hayo yakawa magofu na ukiwa, kama ilivyo leo.’+

7 “Na sasa Yehova, Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Kwa nini mnajiletea msiba mkubwa, ili kila mwanamume na mwanamke, mtoto mdogo na mtoto anayenyonya, waangamie kutoka Yuda, asibaki yeyote? 8 Kwa nini mnikasirishe kwa kazi za mikono yenu kwa kuitolea dhabihu miungu mingine katika nchi ya Misri, ambako mmeenda kukaa? Mtaangamia na kuwa kitu cha kulaaniwa na shutuma miongoni mwa mataifa yote ya dunia.+ 9 Je, mmeyasahau matendo maovu ya mababu zenu na matendo maovu ya wafalme wa Yuda+ na matendo maovu ya wake zao,+ na pia matendo yenu maovu na matendo maovu ya wake zenu,+ yaliyofanywa katika nchi ya Yuda na kwenye barabara za Yerusalemu? 10 Mpaka leo hii hawajajinyenyekeza,* hawajaogopa,+ wala hawajafuata sheria yangu na amri zangu nilizoweka mbele yenu na mbele ya mababu zenu.’+

11 “Kwa hiyo Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Tazameni, nimeazimia kuwaletea msiba, kuiangamiza nchi yote ya Yuda. 12 Nami nitawachukua watu wa Yuda waliobaki walioazimia kwenda nchini Misri kukaa huko, na wote wataangamia nchini Misri.+ Watauawa kwa upanga na kuangamia kwa njaa kali; kuanzia mdogo zaidi mpaka mkubwa zaidi, watakufa kwa upanga na kwa njaa kali. Nao watakuwa laana, kitu cha kutisha, matusi, na shutuma.+ 13 Nitawaadhibu wale wanaoishi nchini Misri kama nilivyoliadhibu Yerusalemu, kwa upanga, kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari.+ 14 Na watu wa Yuda waliobaki ambao wameenda kukaa nchini Misri hawataponyoka wala kuokoka na kurudi kwenye nchi ya Yuda. Watatamani kurudi na kukaa huko, lakini hawatarudi, isipokuwa wachache watakaoponyoka.’”

15 Wanaume wote waliojua kwamba wake zao walikuwa wakiitolea miungu mingine dhabihu na wake wote waliokuwa wamesimama hapo, wakiwa kundi kubwa, na watu wote waliokuwa wakiishi nchini Misri,+ kule Pathrosi,+ wakamjibu hivi Yeremia: 16 “Hatutasikiliza neno ulilotuambia katika jina la Yehova. 17 Badala yake, hakika tutafanya kila neno ambalo vinywa vyetu vimesema, tutamtolea dhabihu Malkia wa Mbinguni* na kummiminia matoleo ya kinywaji,+ kama vile sisi, mababu zetu, wafalme wetu, na wakuu wetu walivyofanya katika majiji ya Yuda na kwenye barabara za Yerusalemu tulipokuwa tumeshiba mkate na tulipokuwa na hali njema, wakati ambapo hatukuona msiba wowote. 18 Tangu tulipoacha kumtolea dhabihu Malkia wa Mbinguni* na kummiminia matoleo ya kinywaji, tumekosa kila kitu nasi tumeangamia kwa upanga na kwa njaa kali.”

19 Wanawake wakasema: “Na tulipokuwa tukimtolea dhabihu Malkia wa Mbinguni* na kummiminia matoleo ya kinywaji, je, tulitengeneza keki za dhabihu zinazofanana naye na kummiminia matoleo ya kinywaji bila idhini ya waume zetu?”

20 Kisha Yeremia akawaambia hivi watu wote, wanaume na wake zao na watu wote waliokuwa wakizungumza naye: 21 “Dhabihu ambazo ninyi, mababu zenu, wafalme wenu, wakuu wenu, na watu wa nchi walitoa katika majiji ya Yuda na kwenye barabara za Yerusalemu+—Yehova alizikumbuka nazo zikaingia moyoni mwake! 22 Mwishowe Yehova hangeweza tena kuvumilia matendo yenu maovu na mambo yenye kuchukiza mliyokuwa mmefanya, nayo nchi yenu ikawa ukiwa, kitu cha kutisha na laana, bila mkaaji, kama ilivyo leo.+ 23 Ni kwa sababu mmetoa dhabihu hizi na kwa sababu mmemtendea dhambi Yehova, kwa kutotii sauti ya Yehova na kutofuata sheria yake, amri zake, na vikumbusho vyake, ndiyo sababu msiba huu umewapata, kama ilivyo leo.”+

24 Yeremia akaendelea kuwaambia hivi watu wote na wanawake wote: “Sikieni neno la Yehova, ninyi nyote watu wa Yuda mlio nchini Misri. 25 Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Mambo ambayo ninyi na wake zenu mmesema kwa vinywa vyenu, mmeyatimiza kwa mikono yenu, kwa maana mlisema: “Hakika tutatimiza nadhiri zetu za kumtolea dhabihu Malkia wa Mbinguni* na kummiminia matoleo ya kinywaji.”+ Hakika ninyi wanawake mtatekeleza nadhiri zenu na kuzitimiza nadhiri zenu.’

26 “Kwa hiyo sikieni neno la Yehova, ninyi nyote watu wa Yuda mnaoishi nchini Misri: ‘“Ninaapa kwa jina langu mwenyewe lililo kuu,” asema Yehova, “kwamba jina langu halitatajwa tena katika kiapo na mtu yeyote wa Yuda+ katika nchi yote ya Misri anayesema, ‘Kwa hakika kama anavyoishi Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova!’+ 27 Sasa ninawatazama ili kuwaletea msiba bali si mema;+ watu wote wa Yuda walio nchini Misri wataangamia kwa upanga na kwa njaa kali, mpaka watakapokwisha kabisa.+ 28 Ni wachache tu watakaoponyoka upanga nchini Misri na kurudi katika nchi ya Yuda.+ Kisha watu wote wa Yuda waliobaki ambao walienda kukaa nchini Misri watajua ni neno la nani lililotimia, langu au lao!”’”

29 “‘Na hii ndiyo ishara kwenu,’ asema Yehova, ‘kwamba nitawaadhibu mahali hapa, ili mjue kwamba maneno niliyosema kuhusu kuwaletea msiba hakika yatatimia. 30 Yehova anasema hivi: “Ninamtia Farao Hofra, mfalme wa Misri, mikononi mwa maadui wake na wale wanaotaka kumuua,* kama nilivyomtia Mfalme Sedekia wa Yuda mikononi mwa Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni, aliyekuwa adui yake na ambaye alitaka kumuua.”’”+

45 Hili ndilo neno ambalo nabii Yeremia alimwambia Baruku+ mwana wa Neria alipoandika katika kitabu maneno haya aliyoambiwa na Yeremia+ katika mwaka wa nne wa utawala wa Yehoyakimu+ mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda:

2 “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi kukuhusu wewe, Baruku, 3 ‘Umesema: “Ole wangu, kwa maana Yehova ameongeza huzuni kwenye maumivu yangu! Nimechoka kwa sababu ya kulia kwa maumivu, nami sijapata mahali pa kupumzika.”’

4 “Mwambie, ‘Yehova anasema hivi: “Tazama! Kile ambacho nimekijenga ninakibomoa, na kile nilichokipanda ninaking’oa—nchi yote.+ 5 Lakini unajitafutia* mambo makuu. Acha kuyatafuta mambo hayo.”’

“‘Kwa maana, niko karibu kuleta msiba dhidi ya wote wenye mwili,’*+ asema Yehova, ‘na popote utakapoenda, nitakupa uhai wako* kuwa nyara.’”*+

46 Hili ndilo neno la Yehova kwa nabii Yeremia kuhusu mataifa:+ 2 Kuhusu Misri,+ kuhusu jeshi la Farao Neko+ mfalme wa Misri, aliyekuwa kando ya Mto Efrati na aliyeshindwa huko Karkemishi na Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni katika mwaka wa nne wa utawala wa Yehoyakimu+ mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda:

 3 “Tayarisheni ngao ndogo* na ngao kubwa,

Na mwende kupigana.

 4 Wafungeni farasi lijamu na mpande juu yake, enyi wapanda farasi.

Shikeni nafasi zenu na mvae kofia zenu.

Sugueni mikuki na mvae makoti yenu ya vita.

 5 ‘Kwa nini ninawaona wameshikwa na hofu?

Wanarudi nyuma, mashujaa wao wamepondwa-pondwa.

Wamekimbia kwa woga, mashujaa wao hawakugeuka.

Kuna hofu kila mahali,’ asema Yehova.

 6 ‘Wenye mbio hawawezi kukimbia, na mashujaa hawawezi kuponyoka.

Kule kaskazini, kwenye ukingo wa Mto Efrati,

Wamejikwaa na kuanguka.’+

 7 Ni nani huyu anayepanda kama Mto Nile,

Kama mito iliyofurika maji?

 8 Misri inakuja kama Mto Nile,+

Kama mito iliyofurika maji,

Nayo inasema, ‘Nitapanda na kuifunika dunia.

Nitaliangamiza jiji na wale wanaokaa humo.’

 9 Pandeni, enyi farasi!

Nendeni kiwazimu, enyi magari!

Acheni mashujaa wasonge mbele,

Kushi na Putu, wanaobeba ngao,+

Na Ludimu,+ wanaobeba na kuupinda* upinde.+

10 “Siku hiyo ni ya Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova wa majeshi, siku ya kisasi ya kulipiza kisasi dhidi ya maadui wake. Na upanga utanyafua na kujishibisha na kunywa damu yao mpaka ushibe, kwa maana Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova wa majeshi, ana dhabihu* katika nchi ya kaskazini kando ya Mto Efrati.+

11 Panda mpaka Gileadi uchukue zeri,+

Ewe bikira, binti ya Misri.

Umezidisha matibabu yako bure tu,

Kwa maana hakuna tiba kwa ajili yako.+

12 Mataifa yamesikia kuhusu aibu yako,+

Na kilio chako kimejaa nchini.

Kwa maana shujaa anajikwaa juu ya shujaa,

Na wote wawili wanaanguka pamoja.”

13 Hili ndilo neno ambalo Yehova alimwambia nabii Yeremia kuhusu kuja kwa Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni kuishambulia nchi ya Misri:+

14 “Lisemeni katika Misri, litangazeni huko Migdoli.+

Litangazeni huko Nofu* na Tahpanhesi.+

Semeni, ‘Shikeni nafasi zenu na mjitayarishe,

Kwa maana upanga utanyafua pande zote kuwazunguka.

15 Kwa nini watu wako wenye nguvu wamefagiliwa mbali?

Walishindwa kusimama imara,

Kwa maana Yehova amewasukuma na kuwaangusha chini.

16 Wanajikwaa na kuanguka kwa wingi.

Wanaambiana:

“Inukeni! Acheni turudi kwa watu wetu na kwenye nchi yetu

Kwa sababu ya upanga ulio katili.”’

17 Huko wametangaza,

‘Farao mfalme wa Misri ni kelele isiyo na maana

Ambaye ameacha nafasi impite.’*+

18 ‘Kwa hakika kama ninavyoishi,’ asema Mfalme, ambaye jina lake ni Yehova wa majeshi,

‘Ataingia* kama Tabori+ kati ya milima

Na kama Karmeli+ kando ya bahari.

19 Tayarisha mzigo wako kwa ajili ya uhamisho,

Ewe binti unayekaa Misri.

Kwa maana Nofu* itakuwa kitu cha kutisha;

Itawashwa moto* na kuachwa bila mkaaji.+

20 Misri ni kama ndama jike anayependeza,

Lakini wadudu wanaouma watamvamia kutoka kaskazini.

21 Hata wanajeshi wake waliokodiwa walio kati yake ni kama ndama waliononeshwa,

Lakini wao pia wamegeuka na kukimbia pamoja.

Walishindwa kusimama imara,+

Kwa maana siku yao ya msiba imewajia,

Wakati wao wa kuadhibiwa.’*

22 ‘Sauti yake ni kama ya nyoka anayenyiririka,

Kwa maana wanamfuata kwa nguvu, wakiwa na mashoka,

Kama wanaume wanaokata miti.*

23 Wataukata msitu wake,’ asema Yehova, ‘ingawa ulionekana hauwezi kupenywa.

Kwa maana ni wengi sana kuliko nzige, nao hawahesabiki.

24 Hakika binti ya Misri ataaibishwa.

Atatiwa mikononi mwa watu wa kaskazini.’+

25 “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Sasa ninamkazia fikira Amoni+ kutoka No,*+ Farao, Misri, miungu yake,+ wafalme wake—naam, Farao na wote wanaomtumaini.’+

26 “‘Nami nitawatia mikononi mwa wale wanaotaka kuwaua, mikononi mwa Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni+ na watumishi wake. Lakini baadaye watu watakaa ndani yake kama zamani,’ asema Yehova.+

27 ‘Lakini wewe, mtumishi wangu Yakobo, usiogope,

Usiwe na hofu, Ee Israeli.+

Kwa maana, nitakuokoa kutoka mbali sana

Na uzao wako* kutoka katika nchi walikopelekwa utekwani.+

Yakobo atarudi na kuwa na utulivu bila usumbufu,

Bila mtu wa kuwaogopesha.+

28 Basi usiogope, mtumishi wangu Yakobo,’ asema Yehova, ‘kwa maana niko pamoja nawe.

Nitayaangamiza kabisa mataifa yote ambako nilikutawanya,+

Lakini wewe sitakuangamiza.+

Nitakutia nidhamu* kwa kiwango kinachofaa,+

Lakini sitakuacha kamwe bila kukuadhibu.’”

47 Hili ndilo neno la Yehova kwa nabii Yeremia kuwahusu Wafilisti,+ kabla ya Farao kushambulia Gaza. 2 Yehova anasema hivi:

“Tazama! Maji yanakuja kutoka kaskazini.

Yatakuwa mto unaofurika.

Nayo yataifunika nchi na kila kitu kilichomo,

Jiji na wale wanaokaa humo.

Wanaume watalia kwa sauti,

Na kila mtu anayeishi katika nchi ataomboleza.

 3 Watakaposikia sauti ya kishindo cha kwato za farasi dume wake,

Watakaposikia kelele za magari yake ya vita

Na mvumo wa magurudumu yake,

Akina baba hata hawatageuka kuwatazama wana wao,

Kwa maana mikono yao italegea,

 4 Kwa sababu siku inayokuja itawaangamiza Wafilisti wote;+

Itamwangamiza kabisa kutoka Tiro+ na kutoka Sidoni+ kila msaidizi aliyebaki.

Kwa maana Yehova atawaangamiza Wafilisti,

Ambao wamebaki wa kisiwa cha Kaftori.*+

 5 Upara* utakuja Gaza.

Ashkeloni limenyamazishwa.+

Ewe uliyebaki katika bonde lao tambarare,*

Utaendelea kujikatakata mpaka lini?+

 6 Aha! Upanga wa Yehova!+

Utanyamaza mpaka lini?

Rudi ndani ya ala yako.

Pumzika na unyamaze.

 7 Upanga unawezaje kukaa kimya

Wakati Yehova ameuamuru?

Ushambulie Ashkeloni na pwani ya bahari,+

Hapo ndipo alipoupa kazi.”

48 Kuhusu Moabu,+ Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi:

“Ole wake Nebo,+ kwa maana ameangamizwa!

Kiriathaimu+ ameaibishwa na kutekwa.

Kimbilio salama limeaibishwa* na kuvunjwavunjwa.+

 2 Hawamsifu tena Moabu.

Kule Heshboni wamepanga njama ya kumwangusha:+

‘Njooni, tumkomeshe asiwe taifa.’

Wewe pia, ewe Madmeni, unapaswa kukaa kimya,

Kwa maana upanga unakufuata.

 3 Kuna sauti ya kilio kutoka Horonaimu,+

Ya uharibifu na anguko kubwa.

 4 Moabu amevunjwa.

Watoto wake wanalia kwa sauti.

 5 Kwenye njia inayopanda kwenda Luhithi wanaendelea kulia huku wakipanda.

Na kwenye njia inayoshuka kutoka Horonaimu wanasikia vilio vya taabu kwa sababu ya msiba.+

 6 Kimbieni, okoeni uhai wenu!*

Ni lazima muwe kama mberoshi nyikani.

 7 Kwa sababu unatumaini kazi zako na hazina zako,

Wewe pia utatekwa.

Na Kemoshi+ atapelekwa uhamishoni,

Pamoja na makuhani wake na wakuu wake.

 8 Mwangamizaji atakuja katika kila jiji,

Na hakuna jiji litakaloponyoka.+

Hakika bonde litaangamia,*

Na nchi tambarare itaharibiwa,* kama alivyosema Yehova.

 9 Mwekeeni Moabu alama,

Kwa maana atakapoanguka na kuwa magofu atakimbia,

Na majiji yake yatakuwa kitu cha kutisha,

Bila mkaaji.+

10 Alaaniwe mtu anayefanya kazi ya Yehova kwa uzembe!

Alaaniwe mtu anayeuzuia upanga wake usimwage damu!

11 Wamoabu hawajasumbuliwa tangu ujana wao,

Kama divai iliyotulia kwenye machicha.

Hawajamiminwa kutoka katika chombo kimoja kwenda kingine,

Nao hawajawahi kamwe kupelekwa uhamishoni.

Ndiyo sababu ladha yao imebaki vilevile,

Na harufu yao haijabadilika.

12 “‘Kwa hiyo tazama! siku zinakuja,’ asema Yehova, ‘nitakapowatuma watu wawapindue. Watawapindua na kumwaga kabisa kile kilicho ndani ya vyombo vyao, nao wataivunja mitungi yao mikubwa vipandevipande. 13 Na Wamoabu wataona aibu kwa sababu ya Kemoshi, kama watu wa nyumba ya Israeli walivyoona aibu kwa sababu ya Betheli, iliyokuwa tegemeo lao.+

14 Mnawezaje kuthubutu kusema: “Sisi ni mashujaa hodari, walio tayari kwa vita”?’+

15 ‘Moabu ameangamizwa,

Majiji yake yamevamiwa,+

Na vijana wao walio bora wamechinjwa,’+

Asema Mfalme, ambaye jina lake ni Yehova wa majeshi.+

16 Msiba wa Wamoabu unakuja hivi karibuni,

Na anguko lao linakaribia upesi.+

17 Wote wanaowazunguka watawasikitikia,

Wote wanaolijua jina lao.

Waambieni hivi: ‘Jinsi fimbo yenye nguvu ilivyovunjwa, fimbo ya urembo!’

18 Shuka chini kutoka kwenye utukufu wako,

Nawe uketi katika kiu,* ewe binti unayekaa Diboni,+

Kwa maana mwangamizaji wa Moabu amekuja kukushambulia,

Ataziharibu sehemu zako zenye ngome.+

19 Simama kando ya barabara utazame, wewe mkaaji wa Aroeri.+

Muulize mwanamume anayekimbia na mwanamke anayeponyoka. ‘Ni nini ambacho kimetokea?’

20 Moabu ameaibishwa na kushikwa na hofu.

Omboleza na ulie kwa sauti.

Tangazeni kule Arnoni+ kwamba Moabu ameangamizwa.

21 “Hukumu imekuja kwenye nchi tambarare,*+ dhidi ya Holoni, Yahazi,+ na Mefaathi;+ 22 dhidi ya Diboni,+ Nebo,+ na Beth-diblathaimu; 23 dhidi ya Kiriathaimu,+ Beth-gamuli, na Beth-meoni;+ 24 dhidi ya Keriothi+ na Bosra; na dhidi ya majiji yote ya nchi ya Moabu, yaliyo mbali na yaliyo karibu.

25 ‘Nguvu za* Moabu zimekatwa;

Na mkono wake umevunjwa,’ asema Yehova.

26 ‘Mlewesheni,+ kwa maana amejikweza dhidi ya Yehova.+

Moabu anagaagaa katika matapishi yake,

Naye ni kitu cha kudhihakiwa.

27 Je, kwako Israeli hakuwa kitu cha kudhihakiwa?+

Je, alipatikana kati ya wezi,

Hivi kwamba utikise kichwa chako na kumshutumu?

28 Ondokeni katika majiji, mkae kwenye jabali, ninyi wakaaji wa Moabu,

Na muwe kama njiwa anayejenga kiota kwenye kuta za korongo.’”

29 “Tumesikia kuhusu kiburi cha Moabu—ana majivuno sana—

Kuhusu kujisifu kwake, kiburi chake, majivuno yake, na jinsi moyo wake ulivyotutumuka.”+

30 “‘Ninajua ghadhabu yake,’ asema Yehova,

‘Lakini maneno yake matupu yatakuwa ya bure.

Hayatafanya chochote.

31 Ndiyo sababu nitaiombolezea Moabu,

Nitalia kwa sauti kwa ajili ya Moabu yote

Na kuwaombolezea wanaume wa Kir-heresi.+

32 Nitakulilia kwa kilio kinachoshinda kilio cha Yazeri,+

Nitakulilia, ewe mzabibu wa Sibma.+

Machipukizi yako yanayositawi yamevuka bahari.

Yamefika mpaka baharini, mpaka Yazeri.

Mwangamizaji ameshuka kwenye

Matunda yako ya wakati wa kiangazi na mavuno yako ya zabibu.+

33 Furaha na shangwe vimeondolewa katika shamba la matunda

Na katika nchi ya Moabu.+

Nimefanya divai iache kutiririka kutoka kwenye shinikizo la divai.

Hakuna mtu atakayelikanyaga shinikizo la divai kwa vigelegele vya shangwe.

Watapaza sauti lakini si kwa shangwe.’”+

34 “‘Kuna kilio kikubwa kutoka Heshboni+ mpaka Eleale.+

Wanapaza sauti yao mpaka Yahazi,+

Kutoka Soari mpaka Horonaimu,+ mpaka Eglath-shelishiya.

Hata maji ya Nimrimu yatabaki ukiwa.+

35 Nitamwondoa kabisa katika Moabu,’ asema Yehova,

‘Mtu anayeleta toleo mahali pa juu

Na mtu anayemtolea dhabihu mungu wake.

36 Ndiyo sababu moyo wangu utaiombolezea* Moabu kama filimbi,*+

Na moyo wangu utawaombolezea* wanaume wa Kir-heresi kama filimbi.*

Kwa kuwa utajiri aliopata utaangamia.

37 Kwa maana kila kichwa kina upara,+

Na ndevu zote zimenyolewa.

Kila mkono umekatwakatwa,+

Nao wamevaa nguo za magunia kiunoni!’”+

38 “‘Juu ya paa zote za Moabu

Na katika viwanja vyake vyote vya jiji,

Hakuna kitu kingine ila maombolezo.

Kwa maana nimemvunja Moabu

Kama chombo kilichotupwa,’ asema Yehova.

39 ‘Jinsi alivyo na hofu! Ombolezeni!

Jinsi Moabu alivyougeuza mgongo wake kwa aibu!

Moabu amekuwa kitu cha kudhihakiwa,

Kitu cha kutisha kwa wote wanaomzunguka.’”

40 “Kwa maana Yehova anasema hivi:

‘Tazama! Kama tai anayeshuka chini kwa ghafla,+

Atanyoosha mabawa yake juu ya Moabu.+

41 Miji itatekwa,

Na ngome zake zitachukuliwa.

Siku hiyo moyo wa mashujaa wa Moabu

Utakuwa kama moyo wa mwanamke anayezaa.’”

42 “‘Na Moabu ataangamizwa asiwe taifa,+

Kwa maana amejikweza dhidi ya Yehova.+

43 Hofu na shimo na mtego viko mbele yako,

Ewe mkaaji wa Moabu,’ asema Yehova.

44 ‘Yeyote anayekimbia hofu ataanguka shimoni,

Na yeyote anayetoka shimoni atanaswa na mtego.’

‘Kwa maana nitawaletea watu wa Moabu mwaka wao wa adhabu,’ asema Yehova.

45 ‘Katika kivuli cha Heshboni, wale wanaokimbia wanasimama wakiwa wameishiwa na nguvu.

Kwa maana moto utatoka Heshboni

Na mwali wa moto utatoka katikati ya Sihoni.+

Utateketeza kabisa paji la uso wa Moabu

Na fuvu la wana wa ghasia.’+

46 ‘Ole wako, ewe Moabu!

Watu wa Kemoshi+ wameangamia.

Kwa maana wana wako wamechukuliwa mateka,

Na mabinti zako wamepelekwa uhamishoni.+

47 Lakini siku za mwisho nitawakusanya watu wa Moabu waliotekwa,’ asema Yehova.

‘Hukumu ya Moabu imefikia hapa.’”+

49 Kuhusu Waamoni,+ Yehova anasema hivi:

“Je, Israeli hana wana:

Je, hana mrithi?

Kwa nini Malkamu+ amemiliki Gadi?+

Na kwa nini watu wake wanaishi katika majiji ya Israeli?”

 2 “‘Kwa hiyo tazameni! siku zinakuja,’ asema Yehova,

‘Nitakapofanya king’ora cha vita kisikike* dhidi ya jiji la Raba+ la Waamoni.+

Atakuwa kilima chenye ukiwa,

Na miji yake itawashwa moto.’

‘Na Israeli atawamiliki wale walioichukua nchi yake,’+ asema Yehova.

 3 ‘Omboleza, ewe Heshboni, kwa maana Ai ameharibiwa!

Lieni kwa sauti, enyi miji ya Raba.

Vaeni nguo za magunia.

Ombolezeni na mzungukezunguke kati ya mazizi ya mawe,*

Kwa maana Malkamu atapelekwa uhamishoni,

Pamoja na makuhani wake na wakuu wake.+

 4 Kwa nini unajigamba kuhusu mabonde,*

Kuhusu eneo lako tambarare linalotiririka, ewe binti usiye mwaminifu,

Unayezitumaini hazina zako

Na unayesema: “Ni nani atakayenishambulia?”’”

 5 “‘Tazama, ninakuletea jambo la kutisha,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova wa majeshi,

‘Kutoka kwa wale wote wanaokuzunguka.

Utatawanywa kila upande,

Na hakuna atakayewakusanya wale wanaokimbia.’”

 6 “‘Lakini baadaye nitawakusanya Waamoni waliotekwa,’ asema Yehova.”

7 Kuhusu Edomu, Yehova wa majeshi anasema hivi:

“Je, hakuna tena hekima yoyote huko Temani?+

Je, ushauri mzuri umetoweka kwa wale walio na uelewaji?

Je, hekima yao imeoza?

 8 Kimbieni, geukeni!

Nendeni mkakae katika sehemu za chini zenye kina, enyi wakaaji wa Dedani!+

Kwa maana nitamletea Esau msiba

Wakati wangu wa kumkazia fikira utakapofika.

 9 Ikiwa wavunaji wa zabibu wangekuvamia,

Je, hawangeacha zabibu chache za kuokotwa?

Kama wezi wangekuja usiku,

Wangesababisha uharibifu kadiri wapendavyo.+

10 Lakini nitamvua Esau awe uchi.

Nitafichua maficho yake,

Ili asiweze kujificha.

Watoto wake na ndugu zake na majirani zake wataangamizwa,+

Naye hatakuwepo tena.+

11 Waache mayatima wako,

Nami nitawahifadhi hai,

Na wajane wako watanitumaini.”

12 Kwa maana Yehova anasema hivi: “Tazama! Ikiwa wale ambao hawajahukumiwa kunywa kikombe lazima wakinywe, je, wewe utaachwa kabisa bila kuadhibiwa? Hutaachwa bila kuadhibiwa, kwa maana lazima ukinywe.”+

13 “Kwa maana nimeapa kwa nafsi yangu mwenyewe,” asema Yehova, “kwamba Bosra litakuwa kitu cha kutisha,+ shutuma, uharibifu, na laana; na majiji yake yote yatakuwa magofu ya kudumu.”+

14 Nimesikia habari kutoka kwa Yehova,

Mjumbe ametumwa kati ya mataifa aseme hivi:

“Jikusanyeni pamoja na mumshambulie;

Jitayarisheni ili kupigana.”+

15 “Kwa maana tazama! Nimekufanya uwe mdogo sana kati ya mataifa,

Umedharauliwa kati ya wanadamu.+

16 Mtetemeko uliosababisha umekudanganya,

Kimbelembele cha moyo wako,

Ewe unayekaa katika mapango ya jabali,

Unayekaa kwenye kilima kirefu zaidi.

Ingawa unajenga kiota chako juu kama tai,

Nitakushusha chini kutoka huko,” asema Yehova.

17 “Na lazima Edomu awe kitu cha kutisha.+ Kila mtu anayepita kando yake atatazama kwa hofu na kupiga mluzi kwa sababu ya mapigo yake yote. 18 Kama Sodoma na Gomora na miji jirani ilivyoangamizwa,”+ Yehova anasema, “hakuna mtu atakayekaa huko, na hakuna mtu atakayeishi huko.+

19 “Tazameni! Kama simba anayetoka kwenye vichaka+ vikubwa kando ya Yordani, mtu fulani atayashambulia malisho yaliyo salama, lakini kwa muda mfupi nitamfanya Edomu akimbie kutoka nchini. Nami nitaweka juu ya nchi hiyo yule aliyechaguliwa. Kwa maana ni nani aliye kama mimi, na ni nani atakayenipinga? Ni mchungaji gani anayeweza kusimama mbele zangu?+ 20 Kwa hiyo sikieni, enyi watu, uamuzi ambao* Yehova amefanya dhidi ya Edomu na mawazo yake dhidi ya wakaaji wa Temani:+

Hakika walio wadogo katika kundi watakokotwa.

Atayafanya makao yao yawe ukiwa kwa sababu yao.+

21 Dunia imetetemeka kwa sauti ya kuanguka kwao.

Kuna kilio kikubwa!

Sauti imesikika mpaka kwenye Bahari Nyekundu.+

22 Tazameni! Atateremka na kushuka kwa ghafla kama tai,+

Naye atanyoosha mabawa yake juu ya Bosra.+

Siku hiyo moyo wa mashujaa wa Edomu

Utakuwa kama moyo wa mwanamke anayezaa.”

23 Kuhusu Damasko:+

“Hamathi+ na Arpadi wameaibishwa,

Kwa maana wamesikia habari mbaya.

Wanayeyuka kwa woga.

Kuna msukosuko baharini ambao hauwezi kutulizwa.

24 Damasko amekufa moyo.

Amegeuka ili kukimbia, lakini ameshikwa na hofu.

Amepatwa na taabu na uchungu,

Kama mwanamke anayezaa.

25 Kwa nini jiji lenye sifa halijaachwa,

Mji wa furaha?

26 Kwa maana vijana wake wataanguka katika viwanja vyake vya jiji,

Na wanajeshi wote wataangamia siku hiyo,” asema Yehova wa majeshi.

27 “Nitauwasha moto ukuta wa Damasko,

Nao utaiteketeza kabisa minara yenye ngome ya Ben-hadadi.”+

28 Kuhusu Kedari+ na falme za Hasori, ambazo Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni alizishambulia na kuzishinda, Yehova anasema hivi:

“Inukeni, pandeni mwende Kedari,

Na muwaangamize wana wa Mashariki.

29 Mahema yao na mifugo yao itachukuliwa,

Vitambaa vyao vya mahema na mali zao zote.

Ngamia wao watachukuliwa,

Nao watawalilia, ‘Kuna hofu kila mahali!’”

30 “Kimbieni, nendeni mbali sana!

Nendeni mkae katika sehemu za chini zenye kina, enyi wakaaji wa Hasori,” asema Yehova.

“Kwa maana Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni ametunga mbinu dhidi yenu,

Naye amefanya mpango wa kuwashambulia.”

31 “Inukeni, shambulieni taifa lililo na amani,

Linalokaa kwa usalama!” asema Yehova.

“Halina milango wala makomeo; wanaishi peke yao.

32 Ngamia wao wataporwa,

Na mifugo yao mingi itakuwa nyara.

Nitawatawanya kwa kila upepo,*

Wale ambao wananyoa nywele pembeni mwa vichwa vyao,+

Nami nitaleta msiba wao kutoka kila upande,” asema Yehova.

33 “Na Hasori atakuwa pango la mbwamwitu,

Ukiwa wa kudumu.

Hakuna mtu atakayekaa huko,

Na hakuna mtu atakayeishi ndani yake.”

34 Hili ndilo neno la Yehova lililomjia nabii Yeremia kuhusu Elamu+ mwanzoni mwa utawala wa Mfalme Sedekia+ wa Yuda: 35 “Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Ninauvunja upinde wa Elamu,+ chanzo cha* nguvu zao. 36 Nitaleta juu ya Elamu zile pepo nne kutoka kwenye miisho minne ya mbingu, nami nitawatawanya kwenye pepo hizi zote. Hakuna taifa ambako watu wa Elamu waliotawanywa hawataenda.’”

37 “Nitawavunjavunja Waelamu mbele ya maadui wao na mbele ya wale wanaotaka kuwaua; nami nitawaletea msiba, hasira yangu inayowaka,” asema Yehova. “Nami nitautuma upanga uwafuate mpaka nitakapowaangamiza kabisa.”

38 “Nami nitaweka kiti changu cha ufalme huko Elamu,+ na huko nitamwangamiza mfalme na wakuu,” asema Yehova.

39 “Lakini siku za mwisho, nitawakusanya watu wa Elamu waliotekwa,” asema Yehova.

50 Neno ambalo Yehova alisema kuhusu Babiloni,+ kuhusu nchi ya Wakaldayo, kupitia nabii Yeremia:

 2 “Semeni jambo hili kati ya mataifa na mlitangaze.

Inueni ishara* na mlitangaze.

Msifiche jambo lolote!

Semeni, ‘Babiloni ametekwa.+

Beli ameaibishwa.+

Merodaki ameshikwa na hofu.

Sanamu zake zimeaibishwa.

Sanamu zake zinazochukiza* zimeshikwa na hofu.’

 3 Kwa maana taifa limemshambulia kutoka kaskazini.+

Linaifanya nchi yake kuwa kitu cha kutisha;

Hakuna mtu anayekaa ndani yake.

Mwanadamu na pia mnyama wamekimbia;

Wameenda zao.”

4 “Siku hizo na wakati huo,” asema Yehova, “watu wa Israeli na watu wa Yuda watakuja pamoja.+ Watatembea wakilia,+ na pamoja watamtafuta Yehova Mungu wao.+ 5 Watauliza njia ya kwenda Sayuni, nyuso zao zikiwa zimeelekezwa upande huo,+ wakisema, ‘Njooni, tujiunge na Yehova katika agano la milele ambalo halitasahauliwa.’+ 6 Watu wangu wamekuwa kundi la kondoo waliopotea.+ Wachungaji wao wenyewe waliwafanya wapotee.+ Waliwapeleka kwenye milima, wakitangatanga kutoka mlima mpaka kilima. Wamepasahau mahali pao pa kupumzika. 7 Wale wote wanaowapata wamewanyafua,+ na maadui wao wamesema, ‘Hatuna hatia, kwa sababu walimtendea dhambi Yehova, walimtendea dhambi Yehova ambaye ni makao ya uadilifu na tumaini la mababu zao.’”

 8 “Kimbieni kutoka Babiloni,

Tokeni katika nchi ya Wakaldayo,+

Na muwe kama wanyama wanaolitangulia kundi.

 9 Kwa maana sasa ninaamsha na kuleta dhidi ya Babiloni

Kusanyiko la mataifa makubwa kutoka katika nchi ya kaskazini.+

Watamshambulia wakiwa wamejipanga kivita;

Kutoka hapo atatekwa.

Mishale yao ni kama ya shujaa

Inayosababisha wazazi wafiwe na watoto;+

Hairudi bila matokeo.

10 Ukaldayo itakuwa nyara.+

Wale wote wanaochukua nyara kutoka kwake watashiba kabisa,”+ asema Yehova.

11 “Kwa maana mliendelea kushangilia,+ mliendelea kufurahi

Mlipokuwa mkiupora urithi wangu mwenyewe.+

Kwa maana mliendelea kukanyagakanyaga kama ndama jike kwenye nyasi,

Nanyi mkaendelea kulia kama farasi dume.

12 Mama yenu ameaibishwa.+

Yule aliyewazaa amekata tamaa.

Tazameni! Yeye ndiye mdogo zaidi kati ya mataifa,

Nyika isiyo na maji na ambayo ni jangwa.+

13 Kwa sababu ya ghadhabu ya Yehova hatakaliwa;+

Atakuwa ukiwa kabisa.+

Yeyote anayepita kando ya Babiloni atatazama kwa hofu

Na kupiga mluzi kwa sababu ya mapigo yake yote.+

14 Mshambulieni Babiloni mkiwa mmejipanga kivita kila upande,

Ninyi nyote mnaoupinda* upinde.

Mpigeni mishale, msiuache mshale wowote,+

Kwa maana amemtendea dhambi Yehova.+

15 Mpigieni kelele za vita kila upande.

Amejisalimisha.*

Nguzo zake zimeanguka, kuta zake zimebomolewa,+

Kwa maana ni kisasi cha Yehova.+

Jilipizieni kisasi dhidi yake.

Mtendeeni kama alivyotenda.+

16 Mkatilieni mbali mpandaji wa mbegu kutoka Babiloni

Na yule anayebeba mundu wakati wa mavuno.+

Kwa sababu ya upanga ulio katili, kila mtu atarudi kwa watu wake mwenyewe,

Kila mtu atakimbilia nchi yake mwenyewe.+

17 “Watu wa Israeli ni kondoo+ waliotawanyika. Simba wamewatawanya.+ Kwanza mfalme wa Ashuru aliwanyafua;+ kisha Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni akaguguna mifupa yao.+ 18 Kwa hiyo Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Nitamtendea mfalme wa Babiloni na nchi yake kama nilivyomtendea mfalme wa Ashuru.+ 19 Nami nitamrudisha Israeli kwenye malisho yake,+ naye atalisha juu ya Karmeli na juu ya Bashani,+ naye atashiba kwenye milima ya Efraimu+ na ya Gileadi.’”+

20 “Siku hizo na wakati huo,” asema Yehova,

“Hatia ya Israeli itatafutwa,

Lakini hakutakuwa na hatia yoyote,

Na dhambi za Yuda hazitapatikana,

Kwa maana nitawasamehe wale nitakaowaacha wabaki.”+

21 “Panda ukashambulie nchi ya Merathaimu na wakaaji wa Pekodi.+

Acha wauawe na kuangamizwa* kabisa,” asema Yehova.

“Fanya yote niliyokuamuru.

22 Kuna sauti ya vita nchini,

Msiba mkubwa.

23 Jinsi nyundo ya chuma ya dunia yote ilivyokatwa na kuvunjwa!+

Jinsi ambavyo Babiloni amekuwa kitu cha kutisha kati ya mataifa!+

24 Nimekutegea mtego, nawe umenaswa, Ee Babiloni,

Nawe hukujua.

Ulipatikana na kukamatwa,+

Kwa maana ulimpinga Yehova.

25 Yehova amefungua ghala lake,

Naye anatoa silaha za ghadhabu yake.+

Kwa maana Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova wa majeshi, ana kazi

Katika nchi ya Wakaldayo.

26 Mshambulieni kutoka sehemu za mbali.+

Fungueni maghala yake.+

Mrundikeni kama marundo ya nafaka.

Mwangamizeni kabisa.+

Naye asiwe na mtu yeyote anayebaki.

27 Waueni ng’ombe dume wake wote wachanga;+

Na washuke kwenda machinjioni.

Ole wao, kwa maana siku yao imefika,

Wakati wao wa kuadhibiwa!*

28 Kuna sauti ya wale wanaokimbia,

Wale wanaoponyoka kutoka nchi ya Babiloni,

Ili kutangaza katika Sayuni kisasi cha Yehova Mungu wetu,

Kisasi kwa ajili ya hekalu lake.+

29 Waiteni wapiga-mishale dhidi ya Babiloni,

Wote wanaoupinda* upinde.+

Pigeni kambi kumzunguka; msiache yeyote aponyoke.

Mlipeni kulingana na matendo yake.+

Mtendeeni kama alivyotenda,+

Kwa maana ametenda kwa kiburi dhidi ya Yehova,

Dhidi ya Mtakatifu wa Israeli.+

30 Basi vijana wake wataanguka katika viwanja vyake vya jiji,+

Na wanajeshi wake wote wataangamia* siku hiyo,” asema Yehova.

31 “Tazama! Niko dhidi yako,+ ewe mkaidi,”+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova wa majeshi,

“Kwa maana lazima siku yako itakuja, wakati ambapo nitakufanya uwajibike.*

32 Wewe, ewe mkaidi, utajikwaa na kuanguka,

Hakutakuwa na mtu wa kukuinua.+

Nami nitayawasha moto majiji yako,

Nao utateketeza kabisa kila kitu kinachokuzunguka.”

33 Yehova wa majeshi anasema hivi:

“Watu wa Israeli na Yuda wamekandamizwa,

Na wale wote wanaowachukua mateka wamewazuilia.+

Wamekataa kuwaachilia waende.+

34 Lakini Mkombozi wao ana nguvu.+

Yehova wa majeshi ndilo jina lake.+

Bila shaka atatetea kesi yao,+

Ili kuipumzisha nchi+

Na kuwafadhaisha wakaaji wa Babiloni.”+

35 “Kuna upanga dhidi ya Wakaldayo,” asema Yehova,

“Dhidi ya wakaaji wa Babiloni na dhidi ya wakuu wake na dhidi ya watu wake wenye hekima.+

36 Kuna upanga dhidi ya wale wanaoongea maneno matupu,* nao watatenda kipumbavu.

Kuna upanga dhidi ya mashujaa wake, nao watashikwa na hofu.+

37 Kuna upanga dhidi ya farasi wao na magari yao ya vita,

Na dhidi ya watu wa mataifa mbalimbali waliochangamana nao,

Nao watakuwa kama wanawake.+

Kuna upanga dhidi ya hazina zake, nazo zitaporwa.+

38 Kuna uharibifu dhidi ya maji yake, nayo yatakaushwa.+

Kwa maana ni nchi ya sanamu za kuchongwa,+

Na kwa sababu ya maono yao yanayotisha wanaendelea kutenda kiwazimu.

39 Kwa hiyo, viumbe wa jangwani watakaa pamoja na wanyama wanaopiga mayowe,

Na mbuni watakaa ndani yake.+

Hakutakuwa na wakaaji tena ndani yake,

Wala watu hawataishi humo kwa vizazi vyote.”+

40 “Kama Mungu alivyoangamiza Sodoma na Gomora+ na miji jirani,”+ asema Yehova, “hakuna mtu atakayekaa huko, na hakuna mtu atakayeishi huko.+

41 Tazama! Watu wanakuja kutoka kaskazini;

Taifa kubwa na wafalme wakuu+ watainuliwa

Kutoka sehemu za mbali zaidi za dunia.+

42 Wanatumia upinde na mkuki.+

Ni wakatili na hawataonyesha rehema.+

Sauti yao ni kama bahari inayovuma,+

Wakiwa wamepanda farasi wao.

Wamejipanga kivita kama mtu mmoja dhidi yako, ewe binti ya Babiloni.+

43 Mfalme wa Babiloni amesikia habari kuwahusu,+

Na mikono yake imelegea.+

Amepata maumivu,

Uchungu kama wa mwanamke anayezaa.

44 “Tazama! Kama simba anayetoka kwenye vichaka vikubwa kando ya Yordani, mtu fulani atayashambulia malisho yaliyo salama, lakini kwa muda mfupi nitawafanya Waedomu wakimbie kutoka nchini. Nami nitaweka juu ya nchi hiyo yule aliyechaguliwa.+ Kwa maana ni nani aliye kama mimi, na ni nani atakayenipinga? Ni mchungaji gani anayeweza kusimama mbele zangu?+ 45 Kwa hiyo sikieni, enyi watu, uamuzi ambao* Yehova amefanya dhidi ya Babiloni+ na mawazo yake dhidi ya nchi ya Wakaldayo.

Hakika walio wadogo katika kundi watakokotwa.

Atayafanya makao yao yabaki ukiwa kwa sababu yao.+

46 Sauti ya kutekwa kwa Babiloni itafanya dunia itetemeke,

Na kilio kitasikika kati ya mataifa.”+

51 Yehova anasema hivi:

“Tazameni, ninaleta upepo unaoharibu

Dhidi ya Babiloni+ na dhidi ya wakaaji wa Leb-kamai.*

 2 Nitawatuma wapepetaji Babiloni,

Nao watampepeta na kuifanya nchi yake kuwa tupu;

Watamshambulia kutoka pande zote siku ya msiba.+

 3 Anayepiga mishale asiupinde* upinde wake.

Na yeyote asisimame akiwa amevaa koti lake la vita.

Msiwahurumie vijana wake.+

Angamizeni jeshi lake lote.

 4 Nao watauawa katika nchi ya Wakaldayo,

Wakiwa wamechomwa kwa silaha katika barabara zake.+

 5 Kwa maana Mungu wa Israeli na Yuda, Yehova wa majeshi, hajawaacha wakiwa wajane.+

Lakini nchi yao* imejaa hatia machoni pa Mtakatifu wa Israeli.

 6 Kimbieni kutoka Babiloni,

Kimbieni ili mwokoe uhai wenu.*+

Msiangamie kwa sababu ya kosa lake.

Kwa maana ni wakati wa kisasi cha Yehova.

Anamlipa kulingana na matendo yake.+

 7 Babiloni amekuwa kikombe cha dhahabu mkononi mwa Yehova;

Aliilewesha dunia yote.

Mataifa yamekunywa divai yake;+

Ndiyo sababu mataifa yameshikwa na wazimu.+

 8 Babiloni ameanguka ghafla, naye amevunjika.+

Mwombolezeeni!+

Leteni zeri kwa ajili ya maumivu yake; labda atapona.”

 9 “Tulijaribu kumponya Babiloni, lakini hakupona.

Mwacheni, twendeni kila mmoja kwenye nchi yake.+

Kwa maana hukumu yake imefika mbinguni;

Iko juu kama mawingu.+

10 Yehova ametutendea haki.+

Njooni, tusimulie katika Sayuni kazi ya Yehova Mungu wetu.”+

11 “Isugueni mishale;+ chukueni ngao za mviringo.*

Yehova ameichochea roho ya wafalme wa Wamedi,+

Kwa sababu anakusudia kuiangamiza Babiloni.

Kwa maana hiki ndicho kisasi cha Yehova, kisasi kwa ajili ya hekalu lake.

12 Inueni ishara*+ dhidi ya kuta za Babiloni.

Imarisheni ulinzi, wekeni walinzi.

Watayarisheni wale wanaovizia.

Kwa maana Yehova ametunga mbinu,

Naye atatekeleza alichoahidi dhidi ya wakaaji wa Babiloni.”+

13 “Ewe mwanamke unayekaa juu ya maji mengi,+

Mwenye hazina nyingi,+

Mwisho wako umefika, kikomo* chako cha kupata faida.+

14 Yehova wa majeshi ameapa kwa nafsi yake,

‘Nitakujaza wanaume wengi kama nzige,

Nao watapiga kelele za ushindi juu yako.’+

15 Yeye ndiye Muumba wa dunia kwa nguvu zake,

Yule aliyeiimarisha ardhi inayozaa kwa hekima yake+

Na aliyezitandaza mbingu kwa uelewaji wake.+

16 Anapofanya sauti yake isikike,

Maji yaliyo mbinguni huwa na msukosuko,

Naye huyafanya mawingu yapande* kutoka kwenye miisho ya dunia.

Hutengeneza radi* kwa ajili ya mvua,

Naye huutoa upepo katika maghala yake.+

17 Kila mtu anatenda bila kutumia akili na bila ujuzi.

Kila fundi wa chuma ataaibishwa kwa sababu ya sanamu ya kuchongwa;+

Kwa maana sanamu yake ya chuma* ni uwongo,

Nazo hazina roho* ndani yake.+

18 Sanamu hizo ni udanganyifu,*+ kazi ya mzaha.

Siku yao ya hukumu itakapofika, zitaangamia.

19 Fungu la Yakobo si kama vitu hivyo,

Kwa maana Yeye ndiye aliyeumba kila kitu,

Hata fimbo ya urithi wake.+

Yehova wa majeshi ndilo jina lake.”+

20 “Wewe ni rungu langu la vita, silaha ya vita,

Kwa maana nitakutumia kuyavunjavunja mataifa.

Nitakutumia kuziangamiza falme.

21 Nitakutumia kumvunjavunja farasi na mpandaji wake.

Nitakutumia kulivunjavunja gari la vita na mwendeshaji wake.

22 Nitakutumia kumvunjavunja mwanamume na mwanamke.

Nitakutumia kumvunjavunja mzee na mvulana.

Nitakutumia kumvunjavunja mwanamume na mwanamke kijana.

23 Nitakutumia kumvunjavunja mchungaji na mifugo yake.

Nitakutumia kumvunjavunja mkulima na kundi lake la wanyama.

Nitakutumia kuwavunjavunja magavana na watawala wasaidizi.

24 Nami nitamlipa Babiloni na wakaaji wote wa Ukaldayo

Kwa sababu ya uovu wote ambao wametenda huko Sayuni mbele ya macho yenu,”+ asema Yehova.

25 “Tazama, niko dhidi yako,+ ewe mlima wa uharibifu,” asema Yehova,

“Wewe unayeiharibu dunia yote.+

Nitaunyoosha mkono wangu dhidi yako na kukubingirisha kutoka kwenye majabali

Na kukufanya uwe mlima ulioteketezwa kabisa.”

26 “Watu hawatachukua kutoka kwako jiwe la pembeni wala jiwe la msingi,

Kwa sababu utabaki ukiwa milele,”+ asema Yehova.

27 “Inueni ishara* katika nchi.+

Pigeni pembe kati ya mataifa.

Wekeni* mataifa ya kumshambulia.

Iteni dhidi yake falme za Ararati,+ Mini, na Ashkenazi.+

Wekeni juu yake ofisa mwandikishaji.

Wafanyeni farasi waje kama nzige wenye miiba.

28 Wekeni* mataifa ya kumshambulia,

Wafalme wa Umedi,+ magavana wake na watawala wake wote wasaidizi

Na nchi zote wanazozitawala.

29 Nayo dunia itatetemeka na kutikisika,

Kwa maana mawazo ya Yehova dhidi ya Babiloni yatatekelezwa

Ili kuifanya nchi ya Babiloni kuwa kitu cha kutisha, bila mkaaji.+

30 Mashujaa wa Babiloni wameacha kupigana.

Wanaketi kwenye ngome zao.

Nguvu zao zimekwisha.+

Wamekuwa kama wanawake.+

Nyumba zake zimewashwa moto.

Makomeo yake yamevunjwa.+

31 Mleta habari mmoja anakimbia kukutana na mleta habari mwingine,

Na mjumbe mmoja kukutana na mjumbe mwingine,

Ili kumjulisha mfalme wa Babiloni kwamba jiji lake limetekwa kila upande,+

32 Kwamba vivuko vimetekwa,+

Kwamba mashua za mafunjo zimeteketezwa kwa moto,

Na kwamba wanajeshi wana hofu.”

33 Kwa maana Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi:

“Binti ya Babiloni ni kama uwanja wa kupuria.

Ni wakati wa kumkanyagia chini awe mgumu.

Hivi karibuni wakati wake wa mavuno utafika.”

34 “Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni ameninyafua;+

Amenivuruga.

Ameniweka chini kama chombo kitupu.

Amenimeza kama nyoka mkubwa;+

Amelijaza tumbo lake kwa vitu vyangu vizuri.

Amenioshea mbali.

35 ‘Babiloni na alipizwe kwa sababu ya ukatili niliotendewa mimi na mwili wangu!’ asema mkaaji wa Sayuni.+

‘Na wakaaji wa Ukaldayo na walipizwe kwa sababu ya damu yangu!’ asema Yerusalemu.”

36 Kwa hiyo Yehova anasema hivi:

“Ninaitetea kesi yako,+

Nami nitakulipizia kisasi.+

Nitaikausha bahari yake na kuvikausha visima vyake.+

37 Na Babiloni atakuwa marundo ya mawe,+

Pango la mbwamwitu,+

Kitu cha kutisha na kitu cha kupigiwa mluzi,

Bila mkaaji.+

38 Wote pamoja watanguruma kama wanasimba.*

Watanguruma kama watoto wa simba.”

39 “Watakapokuwa wamesisimka, nitaandaa karamu yao na kuwalewesha,

Ili wafurahi;+

Kisha watalala usingizi wa kudumu,

Nao hawataamka kutoka katika usingizi huo,”+ asema Yehova.

40 “Nitawashusha chini kama wanakondoo kwenda machinjioni,

Kama kondoo dume pamoja na mbuzi.”

41 “Jinsi Sheshaki* alivyotekwa,+

Jinsi Sifa ya dunia yote ilivyokamatwa!+

Jinsi ambavyo Babiloni amekuwa kitu cha kutisha kati ya mataifa!

42 Bahari imekuja juu ya Babiloni.

Mawimbi yake mengi yamemfunika.

43 Majiji yake yamekuwa kitu cha kutisha, nchi isiyo na maji na jangwa.

Nchi ambayo hakuna mtu atakayeishi wala kupitia humo.+

44 Nitamkazia fikira Beli+ huko Babiloni,

Nami nitatoa kinywani mwake kile alichomeza.+

Mataifa hayatamiminika kwake tena.

Na ukuta wa Babiloni utaanguka.+

45 Tokeni kati yake, watu wangu!+

Kimbieni ili mwokoe uhai wenu*+ kutoka kwa hasira ya Yehova inayowaka!+

46 Msife moyo wala msiogope kwa sababu ya habari itakayosikiwa nchini.

Katika mwaka mmoja habari itakuja,

Na mwaka unaofuata habari nyingine,

Kuhusu ukatili nchini na kuhusu mtawala akimshambulia mtawala mwingine.

47 Kwa hiyo tazama! siku zinakuja

Nitakapozikazia fikira sanamu za kuchongwa za Babiloni.

Nchi yake yote itaaibishwa,

Na watu wake wote waliouawa wataanguka ndani yake.+

48 Mbingu na dunia na vyote vilivyomo

Vitapiga vigelegele vya shangwe kwa sababu ya Babiloni,+

Kwa maana waangamizaji watamvamia kutoka kaskazini,”+ asema Yehova.

49 “Babiloni hakusababisha tu kuuawa kwa Waisraeli walioanguka+

Bali pia huko Babiloni watu waliouawa wa dunia yote wameanguka.

50 Ninyi mnaoponyoka upanga, endeleeni kupiga mwendo, msisimame tuli!+

Mkumbukeni Yehova kutoka mbali,

Yerusalemu na aingie moyoni mwenu.”+

51 “Tumeaibishwa, kwa maana tumesikia dhihaka.

Nyuso zetu zimefunikwa kwa fedheha,

Kwa maana watu wa nchi ya kigeni* wameshambulia mahali patakatifu pa nyumba ya Yehova.”+

52 “Kwa hiyo tazameni! siku zinakuja,” asema Yehova,

“Nitakapozikazia fikira sanamu zake za kuchongwa,

Na katika nchi yake yote waliojeruhiwa watalia kwa maumivu.”+

53 “Hata Babiloni akipanda juu mbinguni,+

Hata akiimarisha ngome zake ndefu,

Watakaomwangamiza watakuja kutoka kwangu,”+ asema Yehova.

54 “Sikilizeni! Kuna kilio kikubwa kutoka Babiloni,+

Sauti ya msiba mkubwa kutoka nchi ya Wakaldayo,+

55 Kwa maana Yehova analiangamiza Babiloni,

Atainyamazisha sauti yake kubwa,

Na mawimbi yao yatavuma kama maji mengi.

Kelele ya sauti yao itasikika.

56 Kwa maana mwangamizaji ataishambulia Babiloni;+

Mashujaa wake watakamatwa,+

Pinde zao zitavunjwavunjwa,

Kwa maana Yehova ni Mungu wa kisasi.+

Bila shaka atalipa kisasi.+

57 Nitawalewesha wakuu wake na watu wake wenye hekima,+

Magavana wake na watawala wake wasaidizi na mashujaa wake,

Nao watalala usingizi wa kudumu,

Nao hawataamka kutoka katika usingizi huo,”+ asema Mfalme, ambaye jina lake ni Yehova wa majeshi.

58 Yehova wa majeshi anasema hivi:

“Ingawa ukuta wa Babiloni ni mpana, utabomolewa kabisa,+

Na ingawa malango yake ni marefu, yatawashwa moto.

Watu watafanya kazi ya bure;

Mataifa yatajichosha ili tu kuuchochea moto.”+

59 Hili ndilo neno ambalo nabii Yeremia alimwamuru Seraya mwana wa Neria+ mwana wa Mahseya alipoenda na Mfalme Sedekia wa Yuda huko Babiloni katika mwaka wa nne wa utawala wake; Seraya alikuwa msimamizi wa makao. 60 Yeremia aliandika katika kitabu kimoja msiba wote ambao ungepata Babiloni, maneno hayo yote yaliyoandikwa dhidi ya Babiloni. 61 Isitoshe, Yeremia akamwambia Seraya: “Utakapofika Babiloni na kuliona jiji hilo, lazima uyasome kwa sauti kubwa maneno haya yote. 62 Kisha useme, ‘Ee Yehova, umesema dhidi ya mahali hapa kwamba pataangamizwa na kubaki bila mkaaji, mwanadamu au mnyama, na kwamba patabaki ukiwa milele.’+ 63 Na utakapomaliza kukisoma kitabu hiki, utakifunga kwenye jiwe na kukitupa katikati ya Mto Efrati. 64 Kisha useme, ‘Hivi ndivyo Babiloni atakavyozama naye hatainuka tena kamwe+ kwa sababu ya msiba ambao ninamletea; nao watachoka.’”+

Maneno ya Yeremia yamefikia hapa.

52 Sedekia+ alikuwa na umri wa miaka 21 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 11 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Hamutali+ binti ya Yeremia kutoka Libna. 2 Aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova, alitenda mambo yote ambayo Yehoyakimu alitenda.+ 3 Mambo hayo yalitukia Yerusalemu na Yuda kwa sababu ya hasira ya Yehova, mpaka alipowatupa mbali kutoka machoni pake.+ Na Sedekia akamwasi mfalme wa Babiloni.+ 4 Katika mwaka wa tisa wa utawala wa Sedekia, katika mwezi wa kumi, siku ya kumi ya mwezi huo, Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni alikuja na jeshi lake lote kushambulia Yerusalemu. Walipiga kambi na kujenga ukuta kulizingira jiji hilo pande zote.+ 5 Nao walilizingira jiji hilo mpaka mwaka wa 11 wa utawala wa Mfalme Sedekia.

6 Katika mwezi wa nne, siku ya tisa ya mwezi huo,+ njaa ilikuwa kali sana jijini, na watu waliokuwemo hawakuwa na chakula.+ 7 Mwishowe sehemu ya ukuta wa jiji ikabomolewa, na wanajeshi wote wakakimbia kutoka jijini wakati wa usiku kupitia lango lililokuwa kati ya kuta mbili karibu na bustani ya mfalme, wakati Wakaldayo walipokuwa wakilizingira jiji; nao wakafuata njia inayoelekea Araba.+ 8 Lakini jeshi la Wakaldayo likamfuatia mfalme, nalo likamfikia Sedekia+ katika jangwa tambarare la Yeriko, na wanajeshi wake wote wakatawanyika na kumwacha. 9 Kisha wakamkamata mfalme na kumpeleka mpaka kwa mfalme wa Babiloni kule Ribla katika nchi ya Hamathi, naye akamhukumu. 10 Na mfalme wa Babiloni akawachinja wana wa Sedekia huku Sedekia akitazama, na pia akawachinja wakuu wote wa Yuda huko Ribla. 11 Kisha mfalme wa Babiloni akampofusha macho Sedekia,+ akamfunga kwa pingu za shaba, akampeleka Babiloni, na kumfunga gerezani mpaka siku aliyokufa.

12 Katika mwezi wa tano, siku ya kumi ya mwezi huo, yaani, mwaka wa 19 wa utawala wa Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni, Nebuzaradani mkuu wa walinzi, aliyekuwa mhudumu wa mfalme wa Babiloni, aliingia Yerusalemu.+ 13 Akateketeza kabisa nyumba ya Yehova,+ nyumba ya* mfalme, na nyumba zote za Yerusalemu; aliteketeza pia kila nyumba kubwa. 14 Na jeshi lote la Wakaldayo lililokuwa pamoja na mkuu wa walinzi lilibomoa kuta zilizozunguka Yerusalemu.+

15 Nebuzaradani mkuu wa walinzi akawapeleka uhamishoni baadhi ya watu wa hali ya chini na watu wengine waliobaki jijini. Pia aliwachukua watu waliojisalimisha kwa mfalme wa Babiloni na pia mafundi stadi waliobaki.+ 16 Lakini Nebuzaradani mkuu wa walinzi aliwaacha baadhi ya watu maskini kabisa nchini ili watunze mashamba ya mizabibu na kufanya kazi za kulazimishwa.+

17 Pia Wakaldayo walivunja vipandevipande nguzo za shaba+ za nyumba ya Yehova na magari+ na Bahari ya shaba,+ vitu vilivyokuwa katika nyumba ya Yehova, nao wakaipeleka shaba yote hiyo Babiloni.+ 18 Walichukua pia ndoo za kuondolea majivu, sepetu, mikasi ya kukatia tambi za taa, mabakuli,+ vikombe,+ na vyombo vyote vya shaba vilivyotumiwa katika utumishi wa hekaluni. 19 Mkuu wa walinzi alichukua mabeseni,+ vyetezo, mabakuli, ndoo za kuondolea majivu, vinara vya taa,+ vikombe, na mabakuli yaliyotengenezwa kwa dhahabu na fedha halisi.+ 20 Shaba yote iliyotumiwa kutengeneza zile nguzo mbili, wale ng’ombe dume 12 wa shaba+ waliokuwa chini ya ile Bahari, na yale magari ambayo Mfalme Sulemani alitengeneza kwa ajili ya nyumba ya Yehova, haingeweza kupimwa uzito.

21 Kuhusu nguzo, kila nguzo ilikuwa na kimo cha mikono 18,* na kamba ya kupimia yenye urefu wa mikono 12 ingeweza kuizunguka;+ unene wake ulikuwa upana wa vidole vinne,* na ndani ilikuwa wazi. 22 Na kifuniko cha nguzo kilikuwa cha shaba; na urefu wa kila kifuniko ulikuwa mikono mitano;+ na wavu pamoja na makomamanga yote yaliyozunguka kifuniko hicho yalitengenezwa kwa shaba. Nguzo ya pili ilifanana na nguzo ya kwanza, pia yale makomamanga. 23 Kulikuwa na makomamanga 96 kandokando; jumla, kulikuwa na makomamanga 100 kuzunguka ule wavu.+

24 Mkuu wa walinzi alimchukua pia Seraya mkuu wa makuhani,+ Sefania+ kuhani wa pili, na walinzi watatu wa milango.+ 25 Pia alimchukua kutoka jijini ofisa mmoja wa makao ya mfalme aliyekuwa msimamizi wa wanajeshi, watu saba waliopatikana jijini walioshirikiana kwa ukaribu na mfalme, na pia mwandishi wa mkuu wa jeshi, aliyewaandikisha watu jeshini, na wanaume 60 kutoka miongoni mwa watu wa kawaida waliokuwa bado jijini. 26 Nebuzaradani mkuu wa walinzi aliwachukua na kuwapeleka kwa mfalme wa Babiloni kule Ribla. 27 Mfalme wa Babiloni aliwapiga na kuwaangamiza huko Ribla+ katika nchi ya Hamathi. Hivyo watu wa Yuda wakapelekwa uhamishoni kutoka katika nchi yao.+

28 Hawa ndio watu ambao Nebukadneza* aliwapeleka uhamishoni: katika mwaka wa 7, Wayahudi 3,023.+

29 Katika mwaka wa 18 wa utawala wa Nebukadneza,*+ watu 832 walichukuliwa kutoka Yerusalemu.

30 Katika mwaka wa 23 wa utawala wa Nebukadneza,* Nebuzaradani mkuu wa walinzi aliwapeleka Wayahudi uhamishoni, watu 745.+

Jumla ya watu 4,600 walipelekwa uhamishoni.

31 Kisha katika mwaka wa 37 tangu Mfalme Yehoyakini+ wa Yuda alipopelekwa uhamishoni, katika mwezi wa 12, siku ya 25 ya mwezi huo, Mfalme Evil-merodaki wa Babiloni, katika mwaka alioanza kutawala, alimwachilia huru Mfalme Yehoyakini wa Yuda na kumtoa gerezani.+ 32 Alizungumza naye kwa fadhili na kukikweza kiti chake cha ufalme juu zaidi kuliko viti vya wafalme wengine waliokuwa pamoja naye Babiloni. 33 Basi Yehoyakini akavua mavazi yake ya gerezani, na sikuzote za maisha yake alikuwa akila kwenye meza ya mfalme. 34 Naye alipewa chakula kwa ukawaida kutoka kwa mfalme wa Babiloni, siku baada ya siku, mpaka siku aliyokufa, siku zote za maisha yake.

Huenda jina hili linamaanisha “Yehova Huinua.”

Au “nilikuchagua.”

Tnn., “kabla hujatoka tumboni.”

Au “nilikuweka kando.”

Au “kijana.”

Tnn., “yule anayeamka.”

Au “chungu cha kupikia chenye mdomo mpana.”

Tnn., “kinachopuliziwa,” kuonyesha moto unaochochewa chini yake.

Tnn., “kujifunga kiuno.”

Au “upendo wako mshikamanifu.”

Au “visiwa vya.”

Au “kuchonga,” inaelekea kwenye mwamba.

Au “Wanasimba wenye manyoya marefu shingoni.”

Au “Memfisi.”

Yaani, kijito cha Mto Nile.

Yaani, Mto Efrati.

Au “katika tamaa ya nafsi yake.”

Tnn., “mwezi wake.”

Au “Nimeipenda miungu ya kigeni.”

Au “ukumbuu wake wa harusi?”

Au “nafsi za maskini.”

Tnn., “Mwarabu.”

Tnn., “paji lenye.”

Tnn., “Sitaufanya uso wangu uanguke juu yako.”

Tnn., “njia zako.”

Au “miungu ya kigeni.”

Au labda, “mume wenu.”

Tnn., “majeshi ya mataifa.”

Tnn., “mwenzake.”

Au “mungu wa aibu amekula.”

Au “nguzo ya ishara.”

Au “Pigeni vifua vyenu.”

Au “atakosa ujasiri.”

Au “watakosa ujasiri.”

Au “upanga umefikia nafsi zetu.”

Tashihisi ya kishairi, ambayo labda inaonyesha sikitiko au huruma.

Yaani, wale wanaolitazama jiji ili wajue wakati wa kushambulia.

Tnn., “matumbo yangu.”

Tnn., “katika kuta za moyo wangu.”

Au “nafsi yangu imesikia.”

Au labda, “sauti ya kelele za vita.”

Au “nguzo ya ishara.”

Au “Wana hekima.”

Au “sitaghairi.”

Au “wanja.”

Au “nafsi yangu imechoka.”

Tnn., “hawakudhoofika.”

Tnn., “vifungo.”

Au “nafsi yangu haipaswi.”

Au labda, “Hayuko.”

Yaani, neno la Mungu.

Tnn., “ninyi watu wajinga msio na moyo.”

Au “nafsi yangu haipaswi.”

Tnn., “Takaseni vita dhidi yake.”

Au “liwajibishwe.”

Au “nafsi yangu itakuacha.”

Tnn., “Sikio lao halijatahiriwa.”

Tnn., “wale waliojaa siku.”

Au “jeraha la kuvunjika.”

Au “mtazipumzisha nafsi zenu.”

Au “waliyakataa mafundisho.”

Tnn., “Uchungu wa kuzaa kama wa.”

Yaani, Yeremia.

Tnn., “Haya ni,” yaani majengo yote ya hekalu.

Au “watoto wasio na baba.”

Au “tangu milele mpaka milele.”

Au “moshi wa dhabihu.”

Tnn., “niliamka mapema na kuzungumza.”

Jina la mungu wa kike aliyeabudiwa na Waisraeli waasi imani; huenda ni mungu wa kike wa uzazi.

Au “wanayenikasirisha; wanayenichokoza.”

Au “ushauri wao.”

Tnn., “kila siku niliamka mapema na kuwatuma.”

Tnn., “waliifanya shingo yao iwe ngumu.”

Tnn., “umekatwa kutoka kinywani mwao.”

Au “ambazo zimewekwa wakfu.”

Au “wimbo wa maombolezo.”

Angalia Kamusi, “Gehena.”

Au “sijawahi kamwe kulifikiria.”

Angalia Kamusi, “Gehena.”

Au “nyakati zake zilizowekwa.”

Au labda, “korongo.”

Au “kuhama.”

Au “mafundisho.”

Au “udanganyifu.”

Au “jeraha la kuvunjika.”

Au “jeraha la kuvunjika.”

Au “mafuta yanayotuliza.”

Au “tabibu.”

Au “nafsi yangu haipaswi.”

Au “wimbo wa maombolezo.”

Au “wameyakataa mafundisho.”

Au “nyimbo za maombolezo.”

Au “wimbo huu wa maombolezo.”

Au “anayejisifu na ajisifu.”

Au “nitamfanya awajibike.”

Au “ubatili.”

Au “tezo yake.”

Au “ubatili.”

Mwanzoni, mstari wa 11 uliandikwa katika Kiaramu.

Au “Huufanya mvuke upande.”

Au labda, “malango.”

Au “sanamu ya kuyeyushwa.”

Au “pumzi.”

Au “ubatili.”

Au “ninawarusha.”

Au “jeraha langu la kuvunjika.”

Inaonekana Yeremia ndiye anayeambiwa.

Au “Na iwe hivyo!”

Tnn., “nilikuwa nikiamka mapema na kuwaonya.”

Au “moshi wa dhabihu.”

Au “mungu wa aibu.”

Yaani, Yeremia.

Yaani, dhabihu zilizotolewa hekaluni.

Au “hisia za ndani kabisa.” Tnn., “figo.”

Au “wanaoitafuta nafsi yako.”

Au “nitawafanya wawajibike.”

Au “kuwajibishwa.”

Au “hisia zao za ndani kabisa.” Tnn., “figo zao.”

Au “Mpendwa wa nafsi yangu.”

Au “mwenye madoadoa.”

Au labda, “Linaomboleza.”

Tnn., “wote wenye mwili.”

Au “Nafsi yangu italia.”

Au “yamezingirwa.”

Au “Mwethiopia.”

Au “wa aibu.”

Au “walio wadogo nchini.”

Au “mitaro; matangi.”

Au “atawafanya wawajibike.”

Au “ubashiri.”

Au “nafsi yako imelichukia.”

Au “nafsi yangu haingewaelekea.”

Au labda, “aina nne za hukumu.” Tnn., “familia nne.”

Au labda, “Unatembea ukirudi nyuma.”

Au “kughairi.”

Au “Nafsi yake inapumua.”

Au labda, “Limeaibishwa na kufedheheshwa.”

Tnn., “Usiniondolee mbali.”

Au “ujumbe wa shutuma.”

Au “utakuwa msemaji wangu.”

Desturi za kipagani za kuomboleza ambazo inaelekea zilifanywa katika nchi ya Israeli iliyoasi imani.

Au “yanatazama njia zao zote.”

Tnn., “maiti za.”

Angalia Kamusi.

Au labda, “Kwa hasira yangu umewashwa kama moto.”

Au “mtu mwenye nguvu.”

Tnn., “Anayefanya mwili wa nyama kuwa mkono wake.”

Au “mtu mwenye nguvu.”

Au “ ni mdanganyifu.”

Au labda, “hauwezi kuponywa.”

Au “hisia za ndani kabisa.” Tnn., “figo.”

Au “lakini si kwa haki.”

Tnn., “wanaoniasi,” inaelekea wanamwasi Yehova.

Au “uwaangamize mara mbili zaidi.”

Tnn., “wakazifanya shingo zao kuwa ngumu.”

Au “kusini.”

Tnn., “kama ilivyokuwa sawa machoni pa mfinyanzi kukitengeneza.”

Au “nitaghairi.”

Au “nitaghairi.”

Tnn., “ninatengeneza.”

Au “moshi wa dhabihu.”

Au “ambazo hazijatengenezwa.”

Au “mafundisho hayatatoweka.”

Tnn., “tumpige kwa ulimi.”

Au “wameichimbia shimo nafsi yangu.”

Au “sijawahi kamwe kulifikiria.”

Au “wanaotafuta nafsi yao.”

Au “wanaotafuta nafsi yao.”

Tnn., “walizifanya shingo zao kuwa ngumu ili wasitii.”

Au “hisia za ndani kabisa.” Tnn., “figo.”

Au “ameiokoa nafsi ya maskini.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “ninawageuzia.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “wanaotafuta nafsi yao.”

Au “nafsi yake.”

Au “ataponyoka na uhai wake.”

Tnn., “nimeukaza uso wangu dhidi ya.”

Au “nchi tambarare ya chini.”

Au “Nitakuadhibu.”

Au “kwenye jumba la kifalme la.”

Tnn., “nitawatakasa.”

Pia anaitwa Yehoahazi.

Tnn., “Uchungu wa kuzaa.”

Pia anaitwa Yehoyakini na Yekonia.

Au “wanaotafuta nafsi yako.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “kwenye nchi ambayo wanaiinulia nafsi yao.”

Au “nchi.”

Tnn., “siku zake.”

Au “mrithi mwadilifu.”

Au “wameasi imani.”

Tnn., “Wanaitia nguvu mikono ya.”

Au “Wanawajaza matumaini ya uwongo.”

Au “Ujumbe unaochosha.” Neno hilo la Kiebrania lina maana mbili: “ujumbe mzito kutoka kwa Mungu” au “kitu kinachochosha.”

Au “ujumbe unaochosha.”

Au “ujumbe unaochosha.”

Au “ujumbe unaochosha.”

Au “Ujumbe unaochosha.”

Au “ujumbe unaochosha.”

Au “Ujumbe unaochosha.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Pia anaitwa Yehoyakini na Yekonia.

Au labda, “wajenzi wa maboma ya ulinzi.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “aliwaambia hivi.”

Tnn., “kuamka mapema na kusema.”

Tnn., “akiamka mapema na kuwatuma.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “nitamwadhibu mfalme wa Babiloni.”

Inaonekana hili ni jina la siri la Babeli (Babiloni).

Tnn., “wote wenye mwili wa nyama.”

Au “mwanasimba mwenye manyoya marefu shingoni.”

Au “uwaambie.”

Au “kuinama.”

Au “nitaghairi.”

Au “mafundisho.”

Tnn., “ambao ninaamka mapema na kuwatuma.”

Au “jumba la.”

Au “ataghairi.”

Au “mlima wa hekalu.”

Au “kilima chenye msitu.”

Au “hakujaribu kuutuliza uso wa Yehova.”

Au “akaghairi.”

Tnn., “yule anayefaa machoni pangu.”

Au “wabashiri.”

Tnn., “lipumzike.”

Au “jumba la.”

Yaani, Bahari ya shaba ya hekalu.

Au “jumba la.”

Tnn., “miaka miwili ya siku.”

Au “Na iwe hivyo!”

Au labda, “wajenzi wa maboma ya ulinzi.”

Au “wabashiri.”

Au labda, “zilizopasuka.”

Tnn., “nikiamka mapema na kuwatuma.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “vyuma vya shingoni.”

Au “kiuno chake.”

Tnn., “ni kuu.”

Tnn., “pingu zako nitazikata.”

Au “wageni kutoka nchi nyingine.”

Au “hawatawafanya.”

Au “Nitakurekebisha.”

Au “jeraha lako la kuvunjika.”

Au “jeraha lako la kuvunjika.”

Au labda, “waheshimiwe.”

Tnn., “kutoa moyo wake kuwa rehani ili anikaribie?”

Au “nimeendelea kukutendea kwa upendo mshikamanifu.”

Au “utaenda kucheza dansi ya wale wanaocheka.”

Au “makorongo ya.”

Au “kumkomboa.”

Au “vitu vizuri kutoka kwa.”

Au “Nafsi yao itakuwa.”

Tnn., “mafuta.”

Au “watoto wake.”

Tnn., “matumbo yangu yamechochewa.”

Au “uzao wa.”

Au “yaliyotiwa ganzi.”

Au labda, “mume.”

Au “Amri za.”

Au “nchi yote tambarare ya chini ya mizoga na ya.”

Au “majivu yenye mafuta,” yaani, majivu yaliyojaa mafuta ya dhabihu.

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “jumba la.”

Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.

Au “mkuu kuhusiana na makusudi yako.”

Tnn., “wote wenye mwili wa nyama.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Tnn., “kuamka mapema na kuwafundisha.”

Angalia Kamusi, “Gehena.”

Tnn., “kuwapitisha.”

Au “sijawahi kamwe kulifikiria.”

Angalia Kamusi.

Au “vitu vyote vizuri ninavyowaahidi.”

Au “mrithi mwadilifu.”

Tnn., “mbegu ya.”

Au “amri za.”

Tnn., “mbegu ya.”

Tnn., “mbegu yake.”

Tnn., “mbegu ya.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Tnn., “leo.”

Au “wanaotafuta nafsi zao.”

Au “wanaotafuta nafsi zao.”

Au “vile vyumba.”

Tnn., “Yonadabu,” ufupisho wa jina Yehonadabu.

Tnn., “Yonadabu,” ufupisho wa jina Yehonadabu.

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Tnn., “niliamka mapema na kuzungumza nanyi.”

Tnn., “nikiamka mapema na kuwatuma.”

Tnn., “Yonadabu,” ufupisho wa jina Yehonadabu.

Au “chumba cha kulia chakula.”

Au “aliyenakili maandishi.”

Au “jumba la.”

Au “Maofisa wote wa makao ya mfalme.”

Nusu ya pili ya Novemba na nusu ya kwanza ya Desemba. Angalia Nyongeza B15.

Tnn., “mbegu yake.”

Pia anaitwa Yehoyakini na Yekonia.

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “msizidanganye nafsi zenu.”

Tnn., “wakamtia katika nyumba ya pingu.”

Tnn., “nyumba ya tangi.”

Au “jumba lake la mfalme.”

Tnn., “atakayeenda.”

Au “nafsi yake.”

Au “ataponyoka na uhai wake.”

Tnn., “mikono.”

Au “ofisa wa makao ya mfalme.”

Au “jumba la.”

Au “jumba la.”

Au “jumba la.”

Au “wanaotafuta nafsi yako.”

Tnn., “ukienda nje.”

Au “nafsi yako itaendelea kuishi.”

Tnn., “usipoenda nje.”

Tnn., “kwenda nje.”

Au “jumba la.”

Tnn., “Watu wa amani yako.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au kulingana na mpangilio tofauti wa maandishi ya Kiebrania, “Nergal-shareza, Samgari-nebo, Sarsekimu, Rabsarisi.”

Au “mchawi mkuu (mnajimu).”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “jumba la.”

Au labda, “wafanye utumishi wa lazima.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “ofisa mkuu wa makao ya mfalme.”

Au “mchawi mkuu (mnajimu).”

Au “nafsi yako itakuwa.”

Au “Utaponyoka na uhai wako.”

Tnn., “nisimame mbele ya.”

Au “aiue nafsi yako.”

Au “aiue nafsi yako.”

Tnn., “wa mbegu ya ufalme.”

Au labda, “dimbwi kubwa.”

Au “nitahuzunika.”

Au “mwende kukaa huko kwa muda.”

Au “nafsi zenu.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “atayawasha moto mahekalu ya.”

Au “bila madhara.”

Au “minara ya.”

Au “Nyumba (Hekalu la) ya Jua,” yaani, Heliopolisi.

Au “mahekalu ya.”

Au “Memfisi.”

Tnn., “nikiamka mapema na kuwatuma.”

Au “hawajahisi wamepondeka.”

Jina la mungu wa kike aliyeabudiwa na Waisraeli waasi imani; huenda ni mungu wa kike wa uzazi.

Jina la mungu wa kike aliyeabudiwa na Waisraeli waasi imani; huenda ni mungu wa kike wa uzazi.

Jina la mungu wa kike aliyeabudiwa na Waisraeli waasi imani; huenda ni mungu wa kike wa uzazi.

Jina la mungu wa kike aliyeabudiwa na Waisraeli waasi imani; huenda ni mungu wa kike wa uzazi.

Au “wanaoitafuta nafsi yake.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “unatarajia.”

Au “watu wote.”

Au “nafsi yako.”

Au “nitaacha uponyoke na uhai wako.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Kwa kawaida ilibebwa na wapiga mishale.

Tnn., “kuukanyaga.”

Au “mauaji.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “Memfisi.”

Tnn., “wakati uliowekwa umpite.”

Yaani, yule atakayeishinda Misri.

Au “Memfisi.”

Au labda, “Itakuwa mahame.”

Au “kuwajibishwa.”

Au “wanaokusanya kuni.”

Yaani, Thebesi.

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Tnn., “mbegu yako.”

Au “Nitakurekebisha.”

Yaani, Krete.

Yaani, watanyoa vichwa vyao kwa kuomboleza na kwa aibu.

Au “nchi yao tambarare ya chini.”

Au “Kilele salama kimeaibishwa.”

Au “nafsi zenu.”

Au “nchi tambarare ya chini itaangamia.”

Au “uwanda utaharibiwa.”

Au labda, “kwenye ardhi kavu.”

Au “uwanda.”

Tnn., “Pembe ya.”

Au “utakuwa na msukosuko kwa ajili ya.”

Yaani, filimbi iliyopigwa wakati wa kuomboleza kwenye mazishi.

Au “utakuwa na msukosuko kwa ajili ya.”

Yaani, filimbi iliyopigwa wakati wa kuomboleza kwenye mazishi.

Au labda, “kelele za vita zisikike.”

Au “mazizi ya kondoo.”

Au “maeneo tambarare ya chini.”

Au “shauri ambalo.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “kila upande.”

Tnn., “mwanzo wa.”

Au “nguzo ya ishara.”

Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.

Tnn., “mnaoukanyaga.”

Tnn., “Amempa mkono wake.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “uwaangamize.”

Au “kuwajibishwa.”

Tnn., “wanaoukanyaga.”

Tnn., “watanyamazishwa.”

Au “wakati ambao nitakuadhibu.”

Au “manabii wa uwongo.”

Au “shauri ambalo.”

Inaonekana hili ni jina la siri la Ukaldayo.

Tnn., “asiukanyage.”

Yaani, nchi ya Wakaldayo.

Au “nafsi yenu.”

Au labda, “jazeni podo.”

Au “nguzo ya ishara.”

Tnn., “kipimo.”

Au “huufanya mvuke upande.”

Au labda, “malango.”

Au “sanamu yake ya kuyeyushwa.”

Au “pumzi.”

Au “ubatili.”

Au “nguzo ya ishara.”

Tnn., “Takaseni.”

Tnn., “Takaseni.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “wanasimba wenye manyoya marefu shingoni.”

Inaonekana hili ni jina la siri la Babeli (Babiloni).

Au “nafsi zenu.”

Au “wageni.”

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Au “jumba la.”

Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.

Upana wa kidole ulilingana na sentimita 1.85 (inchi 0.73). Angalia Nyongeza B14.

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki